Hapo mwanzo, Mungu aliumba mbingu na dunia. Dunia ilikuwa bila umbo na tupu. Giza lilikuwa limefunika vilindi vya maji na roho wa Mungu alikuwa akitanda juu ya maji. Mungu akasema: “Mwangaza ukuwe.” Mwangaza ukakuwa. Mungu akaona kwamba mwangaza ule ni muzuri. Kisha Mungu akatenganisha mwangaza na giza. Mwangaza akauita “Muchana” na giza akaliita “Usiku”. Ikakuwa magaribi na kisha ikakuwa asubui, ndiyo siku ya kwanza. Mungu akasema: “Anga likuwe katikati ya maji, litenge maji sehemu mbili.” Ikakuwa hivyo. Mungu akafanya anga, akatenga maji yanayokuwa juu ya anga na yale yanayokuwa chini ya anga lile. Mungu akaliita anga “Mbingu”. Ikakuwa magaribi na kisha ikakuwa asubui, ndiyo siku ya pili. Mungu akasema: “Maji yanayokuwa chini ya mbingu yakusanyike pahali pamoja, inchi kavu itokee.” Ikakuwa hivyo. Mungu akapaita pahali pakavu “Inchi” na kusanyiko la maji akaliita “Bahari”. Mungu akaona kwamba ni vizuri. Kisha Mungu akasema: “Inchi ioteshe mimea: mimea inayozaa mbegu, na miti inayozaa matunda yenye mbegu za aina yake.” Ikakuwa hivyo. Inchi ikaotesha mimea inayozaa mbegu za aina yake, na miti inayozaa matunda yenye mbegu za aina yake. Mungu akaona kwamba ni vizuri. Ikakuwa magaribi na kisha ikakuwa asubui, ndiyo siku ya tatu. Mungu akasema: “Miangaza ikuwe katika anga, itenge muchana na usiku. Ikuwe vitambulisho kwa kuonyesha nyakati, siku na miaka, na iangae katika anga na kuangazia dunia.” Ikakuwa hivyo. Mungu akafanya miangaza miwili mikubwa: ule mukubwa utawale muchana na ule mudogo utawale usiku. Akafanya nyota vilevile. Mungu akaweka miangaza ile katika anga iangazie dunia, ipate kutawala muchana na usiku, na kutenga mwangaza na giza. Mungu akaona kwamba ni vizuri. Ikakuwa magaribi na kisha ikakuwa asubui, ndiyo siku ya ine. Mungu akasema: “Maji yajae makundi ya viumbe vyenye uzima. Na ndege waruke katika anga.” Mungu akaumba nyama wakubwa sana wa bahari na aina zote za viumbe vyenye uzima vinavyotembea ndani ya maji. Akaumba aina zote za ndege. Mungu akaona kwamba ni vizuri. Mungu akavibariki, akasema: “Muzae, muongezeke, mujaze maji ya bahari, nao ndege waongezeke katika inchi.” Ikakuwa magaribi na kisha ikakuwa asubui, ndiyo siku ya tano. Mungu akasema: “Inchi itoe aina zote za viumbe vyenye uzima: nyama wa kufugwa, viumbe vinavyotambaa na nyama wa pori wa kila aina.” Ikakuwa hivyo. Mungu akafanya aina zote za nyama wa pori, nyama wa kufugwa, na viumbe vinavyotambaa. Mungu akaona kwamba ni vizuri. Kisha Mungu akasema: “Tumufanye mutu kwa mufano wetu, anayefanana nasi, atawale samaki wa bahari, ndege wa anga, nyama wa kufugwa, dunia yote na viumbe vyote vinavyotambaa.” Mungu akaumba mutu kwa mufano wake. Ndiyo, kwa mufano wake Mungu alimwumba. Aliwaumba mwanaume na mwanamuke. Mungu akawabariki na kuwaambia: “Muzae, muongezeke, na mujaze inchi na kuitawala. Mutawale samaki wa bahari, ndege wa anga, na kila kiumbe chenye uzima kinachotembea katika dunia.” Kisha Mungu akasema: “Ninawapa kila mumea katika dunia unaozaa mbegu na kila muti unaozaa matunda yenye mbegu, kwa ajili ya chakula chenu. Nao nyama wote katika dunia, ndege wote wa anga, viumbe vyote vinavyotambaa, kila kiumbe chenye uzima, chakula chao kitakuwa majani yote ya mimea.” Ikakuwa hivyo. Mungu akaona kwamba kila kitu alichofanya ni kizuri kabisa. Ikakuwa magaribi na kisha ikakuwa asubui, ndiyo siku ya sita. Hivi ndivyo mbingu na dunia zilivyokamilika pamoja na vitu vyote vinavyokuwa ndani yake. Kwa siku ya saba Mungu alikuwa amemaliza kazi yake yote aliyofanya. Kwa siku ile ya saba Mungu akapumzika kisha kazi yake yote aliyofanya. Mungu akaibariki siku ya saba na kuitakasa, maana kwa siku hiyo Mungu alipumzika kisha kazi yake yote ya kuumba. Hivi ndivyo mbingu na dunia zilivyoumbwa. Siku ile Yawe Mungu alipoumba mbingu na dunia, hakukukuwa mimea juu ya inchi wala miti haikukuwa imeota maana Yawe Mungu hakukuwa ameinyeshea inchi mvua, wala hakukukuwa mutu wa kuilima. Maji yalitoka ndani ya udongo yakainywesha inchi yote. Halafu Yawe Mungu akamwumba mwanaume kwa udongo, akamupulizia ndani ya pua pumzi ya uzima, na yule mwanaume akakuwa kiumbe chenye uzima. Kisha Yawe Mungu akapanda bustani kule Edeni, upande wa mashariki, na mule akamuweka yule mwanaume aliyemwumba. Yawe Mungu akaotesha kutoka udongo kila aina ya miti ya kupendeza macho na inayofaa kwa chakula. Katikati ya bustani hiyo kulikuwa muti wa uzima na muti wa kujua mazuri na mabaya. Kulikuwa muto kule Edeni uliotiririka maji na kuinywesha ile bustani na kutoka kule muto ule uligawanyika kuwa mito mine. Jina la muto wa kwanza ni Pisoni. Muto ule unazunguka inchi yote ya Havila ambako kuna zahabu. Zahabu ya inchi hiyo ni safi kabisa. Kule vilevile kuna marasi ya bedola na mawe mazuri ya sohamu. Jina la muto wa pili ni Gihoni. Ule unazunguka inchi yote ya Kushi. Jina la muto wa tatu ni Tigre, nao unatiririkia upande wa mashariki wa inchi ya Asuria. Jina la muto wa ine ni Furati. Basi, Yawe Mungu akamutwaa yule mwanaume, akamuweka katika bustani ya Edeni, ailime na kuitunza. Yawe Mungu akamwamuru yule mwanaume: “Unaweza kula matunda ya muti wowote katika bustani. Lakini usikule matunda ya muti wa kujua mazuri na mabaya, maana siku utakapokula matunda ya muti ule, hakika utakufa.” Kisha Yawe Mungu akasema: “Si vizuri huyu mwanaume kuwa peke yake. Nitamufanyia musaidizi wa kumufaa.” Basi, Yawe akaumba kutoka udongo kila nyama wa pori na kila ndege wa anga, halafu akamuletea yule mwanaume aone atawapa majina gani. Na majina aliyowapa viumbe hao, yakakuwa ndiyo majina yao. Basi, yule mwanaume akawapa majina nyama wote wa kufugwa, nyama wa pori na ndege wote wa anga. Lakini hakukupatikana musaidizi wa kumufaa. Basi, Yawe Mungu akamuletea yule mwanaume usingizi muzito, na alipokuwa katika usingizi, akatwaa ubavu wake mumoja na kupafunika pahali pale kwa nyama. Na huo ubavu Yawe Mungu alioutoa kwa yule mwanaume akaufanya kuwa mwanamuke, akamuleta kwa huyo mwanaume. Halafu huyo mwanaume akasema: “Kweli! Huyu ni mufupa kutoka mifupa yangu, na nyama kutoka nyama yangu. Huyu ataitwa ‘Mwanamuke’, kwa sababu ametolewa katika mwanaume. ” Ndiyo maana mwanaume anamwacha baba yake na mama yake, na kuambatana na muke wake, nao wawili wanakuwa mwili mumoja. Huyo mwanaume na muke wake wote walikuwa uchi, lakini hawakuona haya. Nyoka alikuwa mwerevu kuliko nyama wote wa pori walioumbwa na Yawe Mungu. Basi, nyoka akamwambia yule mwanamuke: “Ni kweli Mungu alisema musikule matunda ya muti wowote katika bustani?” Mwanamuke akamujibu yule nyoka: “Tunaweza kula matunda ya miti katika bustani lakini Mungu alisema: ‘Musikule matunda ya muti unaokuwa katikati ya bustani, wala musiuguse. Kama sivyo, mutakufa.’ ” Nyoka akamwambia mwanamuke: “Hamutakufa! Mungu alisema hivyo kwa sababu anajua kwamba mukikula matunda ya muti ule mutafumbuliwa macho, nanyi mutakuwa kama Mungu, mukijua mazuri na mabaya.” Basi, mwanamuke alipoona kwamba muti ule ni muzuri kwa chakula, unavutia macho, na kwamba unafaa kwa kupata hekima, akachuma tunda lake, akakula, akamupa mume wake aliyekuwa pamoja naye, naye vilevile akakula. Mara moja macho yao yakafumbuliwa, wakatambua kwamba wako uchi. Kwa hiyo wakashona majani ya muti wa tini, wakajifanyia nguo. Magaribi mwanaume na muke wake wakasikia Yawe Mungu akitembea katika bustani, nao wakajificha kati ya miti ya bustani, Yawe Mungu asipate kuwaona. Lakini Yawe Mungu akamwita yule mwanaume: “Uko wapi?” Naye akamujibu: “Nilisikia sauti yako katika bustani, nikaogopa maana nilikuwa uchi. Nikajificha.” Yawe akamwuliza: “Nani aliyekuambia kwamba uko uchi? Umekula tunda la muti nililokuamuru usikule?” Yule mwanaume akajibu: “Mwanamuke uliyenipa akae pamoja nami ndiye aliyenipa tunda la muti ule, nami nikakula.” Yawe Mungu akamwuliza yule mwanamuke: “Umefanya nini wewe?” Mwanamuke akamujibu: “Nyoka alinidanganya, nami nikakula.” Kisha Yawe akamwambia nyoka: “Kwa sababu umefanya hivyo, umelaaniwa kuliko nyama wote wa kufugwa, na kuliko nyama wote wa pori. Utatambaa kwa tumbo lako na kula mavumbi siku zote za maisha yako. Nitaweka uadui kati yako na yule mwanamuke, kati ya uzao wako na uzao wake. Yeye ataponda kichwa chako, nawe utamwuma kisigino chake.” Kisha akamwambia mwanamuke: “Nitakuzidishia uchungu wa kuzaa, Utazaa watoto kwa uchungu. Utakuwa na hamu na mume wako, naye atakutawala.” Kisha akamwambia yule mwanaume: “Wewe umemusikiliza muke wako na kula matunda ya muti ambayo nilikuamuru usikule. Basi, udongo umelaaniwa kwa sababu yako. Kwa jasho utajipatia toka humo chakula chako, siku zote za maisha yako. Udongo utakuzalia miiba na magugu, nawe utakula majani ya shamba. Kwa jasho la uso wako utajipatia chakula, mpaka utakaporudi katika udongo, maana ulitwaliwa katika udongo. Wewe ni mavumbi na utarudi katika mavumbi.” Adamu akamupa muke wake jina “Eva”, maana alikuwa mama wa wanadamu wote. Yawe Mungu akawatengenezea Adamu na muke wake nguo za ngozi, akawavalisha. Kisha Yawe Mungu akasema: “Sasa, mwanadamu amekuwa kama mumoja wetu, anajua mazuri na mabaya. Inafaa kumuzuia kula lile tunda la muti wa uzima, maana akilikula ataishi milele.” Basi, Yawe Mungu akamufukuza Adamu inje ya bustani ya Edeni, kusudi alime udongo ambamo alitwaliwa. Alimufukuza inje. Akaweka makerubi upande wa mashariki wa bustani ya Edeni wakiwa na upanga wa moto uliogeuka huku na kule, kwa kulinda njia inayokwenda kwenye muti wa uzima. Adamu akalala na muke wake Eva, naye akapata mimba, akazaa Kaina. Eva akasema: “Nimepata mutoto mwanaume kwa musaada wa Yawe!” Kisha akazaa ndugu yake Abeli. Abeli alikuwa mufugaji wa kondoo na Kaina alikuwa mulimaji. Nyuma ya muda fulani, Kaina akamutolea Yawe sadaka kutoka mazao ya shamba, naye Abeli akamutolea Mungu sadaka ya wazao wa kwanza wa kondoo wake na nyama nono. Yawe akapendezwa na Abeli pamoja na sadaka yake, lakini hakupendezwa na Kaina wala na sadaka yake. Basi, Kaina akakasirika sana na uso wake ukakunjamana. Yawe akamwambia Kaina: “Kwa nini umekasirika, na kwa nini uso wako umekunjamana? Ukitenda vyema hautakubaliwa? Na usipotenda vyema, basi, zambi inajificha kwa mulango; inakutamani, lakini unapaswa kuishinda.” Kisha Kaina akasemezana na ndugu yake Abeli. Basi, walipokuwa katika shamba, Kaina akamushambulia ndugu yake Abeli, akamwua. Yawe akamwuliza Kaina: “Ndugu yako Abeli yuko wapi?” Kaina akamujibu: “Mimi sijui! Mimi ni mulinzi wa ndugu yangu?” Yawe akasema: “Umefanya nini? Damu ya ndugu yako inanililia kutoka katika udongo. Sasa wewe unalaaniwa juu ya udongo ambao ulifungua kinywa kwa kupokea damu ya ndugu yako uliyemwua. Unapolima udongo, hautakupatia tena mazao yake. Utakuwa mukimbizi na mwenye kutangatanga katika dunia.” Kaina akamwambia Yawe: “Azabu yangu ni kubwa sana. Siwezi kuivumilia. Angalia, leo umenifukuza kutoka udongo wenye mboleo na mbali nawe. Basi, nitakuwa mukimbizi na mwenye kutangatanga katika dunia, na yeyote atakayeniona ataniua.” Lakini Yawe akamujibu: “Hapana, sivyo! Atakayekuua wewe Kaina atalipizwa mara saba.” Basi, Yawe akamutia Kaina kitambulisho hata yeyote atakayemwona asimwue. Kisha Kaina akaondoka mbele ya Yawe, akaenda kuishi katika inchi ya Nodi, upande wa mashariki wa Edeni. Kaina akalala na muke wake, naye muke wake akapata mimba, akazaa Enoki. Kaina akajenga muji akauita kwa jina la mwana wake Enoki. Enoki akazaa Iradi, naye Iradi akazaa Mehuyaeli, naye Mehuyaeli akazaa Metusaeli, naye Metusaeli akazaa Lameki. Lameki akaoa wanawake wawili, mumoja aliitwa Ada na mwingine Sila. Ada akazaa Yabali ambaye alikuwa baba ya wafugaji wanaoishi katika mahema. Ndugu yake alikuwa Yubali; huyo alikuwa baba ya wapiga muziki wote wanaopiga zeze na filimbi. Naye Sila akazaa Tubali-Kaina, ambaye alikuwa mufuaji wa vyombo vyote vya shaba na chuma. Dada ya Tubali-Kaina alikuwa Nama. Lameki akawaambia wake zake: “Ada na Sila musikie sauti yangu! Musikilize maneno ninayosema enyi wake za Lameki. Maana niliua mutu kwa sababu ya kunipiga, nilimwua kijana kwa kuniumiza. Ikiwa Kaina atalipizwa mara saba, kweli Lameki atalipizwa mara makumi saba na saba.” Adamu akalala tena na Eva muke wake, naye akazaa mutoto mwanaume, akamwita Seti akisema: “Mungu amenijalia mutoto pahali pa Abeli aliyeuawa na Kaina.” Seti naye akapata mutoto mwanaume, akamwita Enosi. Hapo ndipo watu walipoanza kumwomba Yawe kwa jina lake. Hiki ndicho kitabu cha uzao wa Adamu. Wakati Mungu alipowaumba wanadamu, aliwaumba kwa mufano wake. Aliwaumba mwanaume na mwanamuke, kisha akawabariki na kuwapa jina “Wanadamu” siku ileile alipowaumba. Adamu alipokuwa na umri wa miaka mia moja na makumi tatu, alipata mutoto aliyefanana naye, na mwenye sura kama yake; akamwita Seti. Kisha kuzaa Seti, Adamu akaishi miaka mia nane, na kupata wana wengine na wabinti. Adamu alikufa akiwa na umri wa miaka mia tisa na makumi tatu. Wakati Seti alipokuwa na umri wa miaka mia moja na mitano, akazaa Enosi. Kisha kuzaa Enosi, Seti akaishi miaka mia nane na saba, na kupata wana wengine na wabinti. Seti akakufa akiwa na umri wa miaka mia tisa kumi na miwili. Wakati Enosi alipokuwa na umri wa miaka makumi tisa, akazaa Kenani. Kisha kuzaa Kenani, Enosi akaishi miaka mia nane kumi na mitano, na kupata wana wengine na wabinti. Enosi akakufa akiwa na umri wa miaka mia tisa na mitano. Wakati Kenani alipokuwa na umri wa miaka makumi saba, akazaa Mahalaleli. Kisha kuzaa Mahalaleli, Kenani akaishi miaka mia nane na makumi ine, na kupata wana wengine na wabinti. Kenani alikufa akiwa na umri wa miaka mia tisa na kumi. Wakati Mahalaleli alipokuwa na umri wa miaka makumi sita na mitano, akazaa Yaredi. Kisha kuzaa Yaredi, Mahalaleli akaishi miaka mia nane na makumi tatu, na kupata wana wengine na wabinti. Mahalaleli akakufa akiwa na umri wa miaka mia nane makumi tisa na mitano. Wakati Yaredi alipokuwa na umri wa miaka mia moja makumi sita na miwili, akazaa Henoki. Kisha kuzaa Henoki, Yaredi akaishi miaka mia nane, na kupata wana wengine na wabinti. Yaredi akakufa akiwa na umri wa miaka mia tisa makumi sita na miwili. Wakati Enoki alipokuwa na umri wa miaka makumi sita na mitano, akazaa Metusela. Enoki alikuwa anashirikiana na Mungu. Kisha kuzaa Metusela, Enoki aliishi miaka mia tatu, na kupata wana wengine na wabinti. Enoki aliishi miaka mia tatu makumi sita na mitano. Alikuwa akishirikiana na Mungu, akatoweka, kwa maana Mungu alimupeleka. Wakati Metusela alipokuwa na umri wa miaka mia moja makumi nane na saba, akazaa Lameki. Kisha kuzaa Lameki, Metusela akaishi miaka mia saba makumi nane na miwili, na kupata wana wengine na wabinti. Metusela akakufa akiwa na umri wa miaka mia tisa makumi sita na tisa. Wakati Lameki alipokuwa na umri wa miaka mia moja makumi nane na miwili, akazaa mutoto mwanaume. Akamwita mutoto yule Noa, akisema: “Mutoto huyu ndiye atakayetufariji kutokana na kazi yetu ngumu tunayofanya kwa mikono yetu katika inchi ambayo Yawe alilaani.” Kisha kuzaa Noa, Lameki akaishi miaka mia tano makumi kenda na mitano, na kupata wana wengine na wabinti. Lameki akakufa akiwa na umri wa miaka mia saba makumi saba na saba. Kisha Noa kutimiza umri wa miaka mia tano, akazaa Semu na Hamu na Yafeti. Wakati watu walipoanza kuongezeka katika dunia na kuzaa wabinti, wana wa Mungu wakaona kwamba wale wabinti za watu ni wazuri, wakawatwaa wale waliowapendeza kuwa wake zao. Kwa hiyo, Yawe akasema: “Roho yangu haitakaa ndani ya wanadamu milele, maana yeye ni wa kufa tu. Basi, hataishi zaidi ya miaka mia moja na makumi mbili.” Katika siku zile na hata kisha, kulikuwa majitu katika dunia ambao walikuwa wazao wa wana wa Mungu na wabinti za wanadamu. Hao ndio watu waliokuwa mashujaa na wenye sifa wa zamani, na waliitwa Wanefili. Yawe alipoona uwingi wa uovu wa watu katika dunia, na kwamba kila kitu mwanadamu anachokusudia ndani ya moyo wake ni kiovu siku zote, Yawe akasikitika sana kwa kumwumba mwanadamu katika dunia. Yawe akahuzunika sana ndani ya moyo wake. Hivyo akasema: “Nitamuharibu kabisa katika dunia mwanadamu niliyemwumba, pamoja na nyama wa pori, viumbe vinavyotambaa na ndege wa anga. Ninasikitika kwamba niliwaumba katika dunia.” Lakini Noa akapata kukubaliwa mbele ya Yawe. Hizi ndizo habari za Noa na uzao wake. Noa alikuwa mwenye haki na mukamilifu kati ya watu wa wakati ule. Aliishi katika ushirika na Mungu. Noa alikuwa na wana watatu: Semu, Hamu na Yafeti. Mungu aliona kwamba dunia imeharibika na kujaa mateso makali. Mungu aliangalia dunia, akaona kwamba imeharibika kabisa, kwa maana kila mutu alifuata njia yake mbaya. Mungu akamwambia Noa: “Nimeamua kuwaangamiza wanadamu wote kwa sababu wamejaza dunia mateso makali. Hakika, nitawaangamiza kabisa pamoja na dunia! Kwa hiyo, ujitengenezee chombo kwa mbao ngumu. Gawanya vyumba ndani yake na ukipakae kabulimbo ndani na inje. Utakitengeneza hivi: urefu wake metre mia moja makumi tatu na tatu, upana wake metre makumi mbili na mbili na urefu wake kwenda juu metre kumi na tatu. Chombo hicho kikuwe cha gorofi tatu na chenye mulango pembeni. Utengeneze paa, kisha uache nafasi ya karibu nusu metre kati ya paa na dari. Nitaleta mafuriko ya maji kwa kuangamiza viumbe vyote vyenye uzima katika dunia. Kila kiumbe chenye uzima katika dunia kitakufa. Lakini nitafanya agano nawe. Utaingia katika chombo, wewe pamoja na muke wako, wana wako na wake zao. Nawe utaingiza katika chombo kila aina ya viumbe, wawiliwawili, dume na dike, kwa kuwalinda wazima pamoja nawe. “Utaingiza kila aina ya ndege wa anga, kila aina ya nyama, kila aina ya kiumbe kinachotambaa, wawili wa kila aina, kwa kuwalinda wazima. Utwae vilevile aina zote za vyakula vinavyokuliwa, uvilinde kwa ajili ya chakula chenu na viumbe hivyo.” Noa akafanya yote kama vile Mungu alivyomwamuru. Yawe akamwambia Noa: “Ingia ndani ya chombo wewe pamoja na jamaa yako yote, kwa maana, kati ya watu wote wa kizazi hiki, nimekuona wewe peke yako kuwa mutu wa haki mbele yangu. Utwae pamoja nawe nyama wote wanaohesabiwa kuwa safi, dume saba na dike saba ya kila aina. Lakini nyama wanaohesabiwa kuwa wachafu, utwae dume na dike ya kila aina. Vilevile utwae ndege dume saba na dike saba ya kila aina, kwa kulinda wazima aina zao katika dunia. Nyuma ya siku saba, nitanyesha mvua juu ya inchi siku makumi ine muchana na usiku, na kila kiumbe chenye uzima nilichokiumba katika dunia nitakiangamiza.” Noa akafanya yote kama vile Yawe alivyomwamuru. Noa alikuwa na umri wa miaka mia sita wakati mafuriko ya maji yalipotokea juu ya inchi. Noa, muke wake, wana wake na wake zao wakaingia ndani ya chombo kwa kuepuka mafuriko ya maji. Nyama wanaohesabiwa kuwa safi, nyama wanaohesabiwa kuwa wachafu, ndege na viumbe vyote vinavyotambaa, wawiliwawili, dume na dike, wakaingia ndani ya chombo pamoja na Noa kama vile Mungu alivyomwamuru. Nyuma ya siku saba, maji ya mafuriko yakaanza kuifunika inchi. Noa alipokuwa na umri wa miaka mia sita, katika siku ya kumi na saba ya mwezi wa pili, siku hiyo chemichemi zote za vilindi vya udongo zikabubujika maji, na madirisha ya mbinguni yakafunguka. Mvua ikanyesha juu ya inchi siku makumi ine, muchana na usiku. Siku hiyohiyo mvua ilipoanza kunyesha, Noa, muke wake na wana wake, Semu, Hamu na Yafeti, pamoja na wake zao, wakaingia ndani ya chombo. Waliingia wao wenyewe pamoja na aina zote za nyama wa pori, aina zote za nyama wanaofugwa, aina zote za nyama wanaotambaa na ndege wa kila aina. Wawili wawili wa kila aina ya viumbe vyenye uzima waliingia ndani ya chombo pamoja na Noa. Kila aina yao waliingia dume na dike kama vile Mungu alivyomwamuru Noa. Kisha, Yawe akafunga mulango wa chombo nyuma ya Noa. Mafuriko yalidumu katika inchi kwa muda wa siku makumi ine. Maji yakaongezeka na kuiinua chombo, kikaelea juu ya udongo. Maji yakaendelea kuongezeka zaidi juu ya inchi na chombo kikaelea juu yake. Maji hayo yakakuwa mengi sana juu ya inchi, yakafunika milima yote mirefu katika inchi. Yaliongezeka hata kufunika milima karibu metre saba na nusu. Viumbe vyote vyenye uzima katika inchi vikakufa: ndege, nyama wa kufugwa, nyama wa pori, nyama wadogowadogo katika inchi kavu na wanadamu wote; kila kiumbe chenye uzima katika inchi kavu kilikufa. Mungu akaangamiza kila kiumbe kilichokuwa na pumzi ya uzima katika dunia: wanadamu, nyama, viumbe vinavyotambaa na ndege wa anga. Vyote viliangamizwa katika dunia. Noa tu ndiye aliyebaki na wale waliokuwa pamoja naye ndani ya chombo. Maji hayo yalidumu katika inchi siku mia moja na makumi tano. Kisha Mungu akamukumbuka Noa na nyama wote wa pori na wa kufugwa waliokuwa pamoja naye ndani ya chombo. Basi, Mungu akavumisha upepo juu ya inchi, maji yakaanza kupunguka. Chemichemi za maji ya vilindi na madirisha ya mbinguni yakafungwa. Mvua ikazuiwa, maji yakaendelea kupunguka polepole katika inchi. Nyuma ya siku mia moja na makumi tano, maji yakakuwa yamepunguka sana. Katika siku ya kumi na saba ya mwezi wa saba, chombo ikatua juu ya milima ya Ararati. Maji yakaendelea kupunguka polepole, na siku ya kwanza ya mwezi wa kumi, vilele vya milima vikaonekana. Kisha siku makumi ine, Noa akafungua dirisha alilokuwa ametengeneza katika chombo hicho, akatuma kibombobombo inje, naye hakurudi, lakini aliruka kule na kule mpaka maji yalipokauka katika inchi. Kisha Noa akatuma njiwa apate kuona kama maji yalikuwa yamepunguka juu ya inchi. Lakini kwa vile maji yalikuwa yangali yakifunika inchi yote, yule njiwa hakupata pahali pa kutua, akarudilia Noa katika chombo. Noa akanyoosha mukono, akamutwaa na kumurudisha ndani ya chombo. Noa akangoja siku zingine saba, kisha akatuma tena yule njiwa. Njiwa yule akamurudilia Noa saa za magaribi akiwa na tawi bichi la muzeituni katika midomo yake. Kwa hiyo Noa akajua kwamba maji yalikuwa yamepunguka katika inchi. Kisha akangoja siku zingine saba, akatuma tena yule njiwa; mara hii, njiwa hakurudi kabisa. Noa alipokuwa na umri wa miaka mia sita na moja, siku ya kwanza ya mwezi wa kwanza, maji yalikuwa yamekauka katika inchi. Noa akafunua kifuniko cha chombo, na alipoangalia, akaona kwamba inchi ilikuwa imekauka. Siku ya makumi mbili na saba ya mwezi wa pili, inchi ilikuwa imekauka kabisa. Hapo, Mungu akamwambia Noa: “Toka katika chombo, wewe pamoja na muke wako, wana wako na wake zao. Ondoa vilevile viumbe vyote vyenye uzima vya kila aina vilivyokuwa pamoja nawe, ndege na nyama na kila kiumbe kinachotambaa, vipate kuzaa kwa wingi katika dunia, viongezeke na kuenea kila pahali katika dunia.” Basi, Noa akatoka katika chombo pamoja na wana wake na muke wake pamoja na wake za wana wake. Wakatoka, kufuatana na jamii zao, nyama wote wa pori, viumbe vyote vinavyotambaa, ndege wote na nyama wote wenye uzima katika dunia. Noa akamujengea Yawe mazabahu, akatwaa mumoja katika kila aina ya nyama wanaohesabiwa kuwa safi na ndege anayehesabiwa kuwa safi, akamutolea Mungu sadaka za kuteketezwa kwa moto juu ya mazabahu. Harufu nzuri ya sadaka hiyo ikamupendeza Yawe, naye akasema ndani ya moyo wake: “Sitailaani tena inchi hata kidogo kwa sababu ya mwanadamu. Ninajua kwamba mawazo yake ni maovu tangu utoto wake. Wala sitaangamiza tena viumbe vyote kama vile nilivyofanya. Kwa kadiri inchi itakavyodumu, wakati wa kupanda na kuvuna, wa baridi na joto, wa mvua na kipwa, usiku na muchana, havitakosa kuwa.” Mungu akamubariki Noa na wana wake, akiwaambia: “Muzae, muongezeke, mujaze inchi. Nyama wote, ndege wote wa anga, viumbe vyote vinavyotambaa juu ya inchi na samaki wote wa bahari watakuwa na hofu na kuwaogopa ninyi. Wote wamewekwa chini ya mamlaka yenu. Nyama wote wenye uzima watakuwa chakula chenu; ninawapa nyama hao kama vile nilivyowapa mimea kuwa chakula chenu. Lakini musikule nyama wenye damu, maana uzima uko katika damu. Damu ya uzima wenu nitaidai. Nitaidai kutoka kwa kila nyama na mwanadamu. Atakayemwua mwanadamu mwenzake, nitamudai uzima wake. Anayemwanga damu ya mwanadamu, damu yake itamwangwa na mwanadamu; maana mwanadamu aliumbwa kwa mufano wa Mungu. Nanyi muzae, mwongezeke, muzae kwa wingi, mwongezeke katika inchi.” Kisha Mungu akamwambia Noa na wana wake: “Ninasimamisha agano langu nanyi na wazao wenu na viumbe vyote vyenye uzima, ndege, nyama wa kufugwa na wa pori, wote waliotoka katika chombo pamoja nanyi. Ninasimamisha agano langu nanyi, kwamba hakutatokea tena mafuriko ya maji kwa kuangamiza inchi nzima au viumbe vyote vyenye uzima.” Tena Mungu akasema: “Hiki ndicho kitambulisho cha agano ninalofanya kati yangu nanyi na kila kiumbe chenye uzima kinachokuwa pamoja nanyi kwa vizazi vyote vinavyokuja: ninaweka upinde wangu katika mawingu, nao utakuwa kitambulisho cha agano kati yangu na dunia. Kila mara nitakapofunika dunia kwa mawingu, na huo upinde wa mvua utakapoonekana katika mawingu, nitakumbuka agano langu nanyi na viumbe vyote vyenye uzima. Maji hayatageuka hata kidogo kuwa mafuriko ya kuangamiza viumbe vyote vyenye uzima. Huo upinde utakapotokea katika mawingu, nitauona na kukumbuka agano hilo la milele kati yangu na viumbe vyote vyenye uzima katika dunia.” Mungu akamwambia Noa: “Hiki ndicho kitambulisho cha agano ambalo nimesimamisha na viumbe vyote vyenye uzima katika dunia.” Wana wa Noa waliotoka katika chombo walikuwa Semu, Hamu na Yafeti. Hamu alikuwa baba ya Kanana. Hao ndio wana watatu wa Noa na kutokana nao watu walienea katika dunia yote. Noa alikuwa mulimaji wa kwanza kupanda mizabibu. Akakunywa divai, akalewa, kisha akalala uchi ndani ya hema yake. Hamu, baba ya Kanana, akaona uchi wa baba yake, akatoka inje na kuwaambia wandugu zake wawili. Lakini Semu na Yafeti wakatwaa nguo, wakaiweka juu ya mabega yao, wakakwenda kinyumenyume na kufunika uchi wa baba yao. Waliangalia pembeni, wala hawakuuona uchi wa baba yao. Ulevi wa Noa ulipokwisha naye alipojua alivyotendewa na mwana wake mudogo, akasema: “Kanana alaaniwe! Atakuwa mutumwa wa watumwa kwa wandugu zake.” Tena akasema: “Semu abarikiwe na Yawe, Mungu wangu! Kanana akuwe mutumwa wake. Mungu amuzidishe Yafeti, aishi katika hema za Semu; Kanana akuwe mutumwa wake.” Nyuma ya mafuriko ya maji, Noa aliishi miaka mia tatu na makumi tano, kisha akakufa akiwa na umri wa miaka mia tisa na makumi tano. Nyuma ya mafuriko ya maji, Semu, Hamu na Yafeti, wana wa Noa, walipata watoto wanaume na wanawake. Hawa ndio wazao wao: Wana wa Yafeti walikuwa Gomeri, Magogi, Madayi, Yavani, Tubali, Meseki na Tirasi. Wana wa Gomeri walikuwa Askenazi, Rifati na Togarma. Wana wa Yavani walikuwa Elisa, Tarsisi, Kitimu na Rodanimu. Kutokana na hawa visanga vya watu wa mataifa mengine vikagawanywa kwa inchi zao, kila watu kwa luga yao, kwa jamaa zao, kufuatana na mataifa yao. Wana wa Hamu walikuwa Kushi, Misiraimu, Puti na Kanana. Wana wa Kushi walikuwa Seba, Havila, Sabuta, Rama na Sabuteka. Wana wa Rama walikuwa Seba na Dedani. Kushi alikuwa baba ya Nimurodi ambaye alikuwa shujaa wa kwanza katika dunia. Alikuwa mwindaji shujaa mbele ya Yawe, ndiyo maana kuna musemo unaosema: “Kama vile Nimurodi mwindaji shujaa mbele ya Yawe.” Miji ya kwanza ya utawala wake ilikuwa Babeli, Ereki, na Akadi katika inchi ya Sinari. Kutoka kule, Nimurodi alikwenda Asuria, akajenga miji ya Ninawe, Rehoboti-Iri, Kala na Reseni unaokuwa kati ya Ninawe na muji mukubwa wa Kala. Misiraimu alikuwa babu ya Waludi, Waanamu, Walehabi, Wanafutuhi, Wapatirusi, Wakasiluhi (ambao ndio shina ya Wafilistini), na Wakafutorimu. Kanana alikuwa babu ya Sidona, muzaliwa wake wa kwanza, na Heti, na vilevile babu ya Wayebusi, Waamori, Wagirgasi, Wahivi, Waarki, Wasini, Waarwadi, Wazemari na Wahamati. Na nyuma watu wa jamaa mbalimbali za Kanana wakatawanyika, hata eneo la inchi yao likakuwa toka Sidona kuelekea upande wa kusini, kuendelea Gerari mpaka Gaza, na kuelekea upande wa mashariki liliendelea kwa Sodoma na Gomora, Adima na Seboimu mpaka Lasa. Hao ndio wazao wa Hamu kufuatana na makabila yao, luga zao, inchi zao na mataifa yao. Semu, mukubwa wa Yafeti, alikuwa baba ya Waebrania wote. Wana wa Semu walikuwa Elamu, Asuri, Aripakisadi, Ludi na Aramu. Wana wa Aramu walikuwa Usi, Huli, Geteri na Masi. Aripakisadi alizaa Sela, Sela akazaa Eberi. Eberi alikuwa na wana wawili: wa kwanza akamwita Pelegi kwa sababu wakati ule watu katika dunia waligawanyika na wa pili akamwita Yokitani. Yokitani alikuwa baba ya Almodadi, Selefu, Hazarimaweti, Yera, Hadoramu, Uzali, Dikela, Obali, Abimaeli, Seba, Ofiri, Havila na Yobabu. Hao wote walikuwa wana wa Yokitani. Inchi walimokaa ilienea toka Mesa mpaka Sefari katika inchi ya vilima vya upande wa mashariki. Hao ndio wazao wa Semu, kufuatana na makabila yao, luga zao, inchi zao na mataifa yao. Hao ndio jamaa za wana wa Noa, kufuatana na vizazi vyao na mataifa yao. Kutokana nao, mataifa yote yalienea katika dunia nyuma ya mafuriko ya maji. Watu wote katika dunia walikuwa na luga moja, walitumia maneno mamoja. Basi, wakati watu waliposafirisafiri toka mashariki, wakafika katika inchi ya mabonde kule Sinari, wakakaa. Kisha wakaambiana: “Tufanye matofali, tuyachome kwa moto vizuri.” Walikuwa na matofali pahali pa mawe, na kabulimbo pahali pa chokaa. Wakasema: “Tujijengee muji na munara ambao chongo yake itafika mbinguni kusudi tujipatie sifa, kusudi tusisambazwe katika dunia yote.” Halafu Yawe akashuka chini kuona muji ule na munara ambayo wanadamu walijenga. Yawe akasema: “Watu hawa ni taifa moja na wote wana luga moja; huu ni mwanzo tu wa yale watakayofanya. Jambo lolote wanalokusudia kufanya watafanikiwa. Basi, tushuke chini na kuvuruga luga yao kusudi wasielewane wao kwa wao.” Hivyo, Yawe akawatawanya pahali pote katika dunia, nao wakaacha kujenga ule muji. Muji ule ukaitwa Babeli, kwa sababu kule ndiko Yawe alikovuruga luga ya dunia yote, na tokea kule akawatawanya watu kila pahali katika dunia. Hawa ndio wazao wa Semu. Miaka miwili nyuma ya yale mafuriko ya maji, Semu akiwa na umri wa miaka mia moja, alizaa Aripakisadi. Nyuma ya kuzaa Aripakisadi, Semu aliishi miaka mia tano, na kupata wana wengine na wabinti. Aripakisadi alipokuwa na umri wa miaka makumi tatu na mitano, akazaa Sela. Nyuma ya kuzaa Sela, Aripakisadi aliishi miaka mia ine na mitatu, na kupata wana wengine na wabinti. Sela alipokuwa na umri wa miaka makumi tatu, alizaa Eberi. Kisha kuzaa Eberi, Sela aliishi miaka mia ine na mitatu, na kupata wana wengine na wabinti. Eberi alipokuwa na umri wa miaka makumi tatu na mine, akazaa Pelegi. Kisha kuzaa Pelegi, Eberi aliishi miaka mia ine na makumi tatu, na kupata wana wengine na wabinti. Pelegi alipokuwa na umri wa miaka makumi tatu, akazaa Reu. Kisha kuzaa Reu, Pelegi aliishi miaka mia mbili na tisa, na kupata wana wengine na wabinti. Reu alipokuwa na umri wa miaka makumi tatu na miwili, akazaa Serugi. Kisha kuzaa Serugi, Reu aliishi miaka mia mbili na saba, na kupata wana wengine na wabinti. Serugi alipokuwa na umri wa miaka makumi tatu, akazaa Nahori. Kisha kuzaa Nahori, Serugi aliishi miaka mia mbili, na kupata wana wengine na wabinti. Nahori alipokuwa na umri wa miaka makumi mbili na tisa, akazaa Tera. Kisha kuzaa Tera, Nahori aliishi miaka mia moja kumi na tisa, na kupata wana wengine na wabinti. Tera alipokuwa na umri wa miaka makumi saba, akazaa Abramu, Nahori, na Harani. Hawa ndio wazao wa Tera, baba ya Abramu, Nahori na Harani. Harani alikuwa baba ya Loti. Huyo Harani alikufa wakati baba yake Tera alikuwa anaishi kule Uri, muji wake wa kuzaliwa. Abramu na Nahori wakaoa. Muke wa Abramu aliitwa Sarai. Muke wa Nahori aliitwa Milka, binti ya Harani ambaye vilevile alikuwa baba ya Isika. Sarai hakukuwa na mutoto kwa sababu alikuwa tasa. Tera akatwaa Abramu mwana wake, Loti mujukuu wake aliyekuwa mwana wa Harani, na Sarai muke wa Abramu, wakaondoka wote pamoja toka Uri, muji wa Wakaldea, na kwenda katika inchi ya Kanana. Lakini walipofika Harani, wakakaa pale. Tera akakufia kule Harani akiwa na umri wa miaka mia mbili na mitano. Basi, Yawe akamwambia Abramu: “Ondoka katika inchi yako, acha jamaa yako na nyumba ya baba yako, uende katika inchi nitakayokuonyesha. Nitakufanya wewe kuwa taifa kubwa, nitakubariki na kutukuza jina lako, nawe utakuwa baraka. Anayekubariki, nitamubariki, anayekulaani, nitamulaani. Kwa njia yako, nitabariki mataifa yote ya dunia.” Kwa hiyo, Abramu akaondoka kama vile Yawe alivyomwamuru, na Loti akakwenda pamoja naye. Abramu alikuwa na umri wa miaka makumi saba na mitano alipotoka Harani. Alitwaa Sarai muke wake, na Loti mwana wa ndugu yake, pamoja na mali yao yote na watu wote waliokuwa wamejipatia kule Harani, wakaondoka kuelekea inchi ya Kanana. Walipoingia katika inchi ya Kanana, Abramu akapita katikati ya inchi mpaka Sekemu, pahali patakatifu, penye muti wa mwelo wa More. Wakati ule, Wakanana walikuwa ndio wenyeji wa inchi hiyo. Halafu Yawe akamutokea Abramu, akamwambia: “Nitawapa wazao wako inchi hii.” Basi, Abramu akajenga mazabahu kwa ajili ya Yawe aliyemutokea. Kisha Abramu akaondoka, akaelekea kwenye mulima upande wa mashariki ya Beteli akapiga hema kati ya muji wa Beteli, upande wa magaribi, na muji wa Ai upande wa mashariki. Pale vilevile akamujengea Yawe mazabahu na kumwomba kwa jina lake. Kisha Abramu akaendelea kusafiri kuelekea upande wa Negebu. Wakati ule, njaa ikatokea katika inchi. Njaa hiyo ilikuwa kali, hivyo Abramu akalazimika kwenda Misri kukaa kule kwa muda. Alipokaribia Misri, Abramu akamwambia Sarai muke wake: “Ninajua kwamba wewe ni mwanamuke muzuri na wa kuvutia. Wamisri watakapokuona watasema: ‘Huyu ni muke wake’, kisha wataniua lakini wewe watakuacha muzima. Basi, uwaambie kwamba wewe ni dada yangu kusudi mambo yaniendee vema, niachwe niishi kwa ajili yako.” Basi, Abramu alipofika Misri, wenyeji wa kule wakaona kwamba Sarai ni mwanamuke muzuri sana. Wakubwa wa mufalme wa Misri walipomwona Sarai, wakamusifia kwa mufalme. Basi, Sarai akapelekwa ndani ya nyumba ya yule mufalme. Naye akamutendea Abramu mema kwa ajili ya Sarai. Akamupa kondoo, ngombe, punda dume, watumishi na wajakazi, punda dike na ngamia. Lakini Yawe akamutesa na watu wote wa nyumba yake kwa mapigo makali kwa sababu ya Sarai, muke wa Abramu. Mufalme akamwita Abramu, akamwuliza: “Ni kitu gani hiki ulichonitendea? Mbona haukunijulisha kwamba Sarai ni muke wako? Kwa nini ulisema ni dada yako hata nikamutwaa kuwa muke wangu? Basi, sasa muke wako ule. Umutwae, ujiendee!” Kisha mufalme yule akawaamuru watu wake wasindikize Abramu katika njia akikuwa na muke wake na mali yake yote. Abramu akarudi kutoka Misri, akaingia upande wa Negebu. Alikuwa na muke wake na mali yake yote pamoja na Loti. Wakati ule, Abramu alikuwa ametajirika sana. Alikuwa na makundi ya nyama, feza na zahabu. Akaendelea kusafiri toka eneo la Negebu mpaka Beteli. Alifika pahali alipokuwa amepiga kambi ya hema mara ya kwanza kati ya Beteli na Ai, pahali ambapo alikuwa amejenga mazabahu. Pale Abramu akamwomba Yawe kwa jina lake. Na Loti, ambaye alikwenda pamoja na Abramu, alikuwa na kondoo, na makundi mengi ya nyama na hema. Hesabu ya nyama wao ilikuwa kubwa sana hata inchi ile haikuweza kutosha kwa Abramu na Loti kuishi pamoja. Basi, kukatokea ugomvi kati ya wachungaji wa Abramu na wachungaji wa Loti. Wakati ule, Wakanana na Waperizi ndio waliokuwa wenyeji wa inchi hiyo. Basi, Abramu akamwambia Loti: “Kusikuwe ugomvi kati yetu wala kati ya wachungaji wako na wachungaji wangu, kwa sababu sisi ni jamaa moja. Angalia inchi hii yote mbele yako. Na tutengane. Ukikwenda kushoto, mimi nitakwenda kuume. Ukikwenda kuume, mimi nitakwenda kushoto.” Loti akainua macho yake, akaona bonde la muto Yordani, akaona kwamba lina maji ya kutosha kila pahali, kama vile bustani ya Yawe na kama vile inchi ya Misri upande wa Soari. (Hii ilikuwa mbele Yawe hajaiangamiza miji ya Sodoma na Gomora). Kwa hiyo, Loti akajichagulia bonde lote la muto Yordani, akaelekea upande wa mashariki, na hivyo wakatengana. Abramu akabaki katika inchi ya Kanana na Loti akakaa kati ya miji iliyokuwa katika bonde, akahamishia kambi yake Sodoma. Watu wa Sodoma walikuwa waovu na watenda zambi wakubwa mbele ya Yawe. Nyuma ya Loti kujitenga na Abramu, Yawe akamwambia Abramu: “Inua macho yako toka pale unapokuwa, utazame pande zote: kaskazini, kusini, mashariki na magaribi. Inchi hii yote unayoona nitakupa wewe na wazao wako ikuwe yenu milele. Wazao wako nitawafanya wakuwe wengi wasihesabike, kama vile mavumbi ya inchi. Kama vile vumbi isivyoweza kuhesabika, ndivyo wazao wako hawataweza kuhesabika! Basi, simama uitembelee inchi hii katika upana na urefu, maana nitakupa wewe inchi ile.” Kwa hiyo, Abramu akaongoa hema, akakwenda kukaa karibu na mielo ya Mamure kule Hebroni. Kule akajengea Yawe mazabahu. Kwa wakati ule, mufalme Amurafeli wa Sinari, mufalme Arioki wa Elasari, mufalme Kedorilaomeri wa Elamu na mufalme Tidali wa Goimu, wakapigana vita na Bera mufalme wa Sodoma, na Birsa mufalme wa Gomora, Sinabu mufalme wa Adima, Semeberi mufalme wa Seboimu, na mufalme wa Bela ni kusema Soari. Wafalme wale watano waliyaunganisha majeshi yao katika bonde la Sidimu, ni kusema bahari ya Chumvi. Kwa muda wa miaka kumi na miwili walikuwa wakimutii mufalme Kedorilaomeri, lakini katika mwaka wa kumi na tatu, wakamwasi. Katika mwaka wa kumi na ine, mufalme Kedorilaomeri na wale wafalme wenzake wakakuja na kuwashinda watu wa Refaimu kule Astaroti-Karnaimu, Wazuzi kule Hamu, Waemi kule Sawe-Kiriataimu, na Wahori kule kwenye mulima wa Seiri, wakawafukuza mpaka Eliparani, kwa mupaka wa jangwa. Kisha wakarudi nyuma mpaka Enimisipati ni kusema Kadesi, wakapiga inchi yote ya Waamaleki, na kuwashinda Waamori waliokaa Hasasoni-Tamari. Halafu mufalme wa Sodoma, mufalme wa Gomora, mufalme wa Adima, mufalme wa Seboimu na mufalme wa Bela ni kusema Soari, wakaingia katika vita katika bonde la Sidimu kupigana na Kedorilaomeri mufalme wa Elamu, Tidali mufalme wa Goimu, Amurafeli mufalme wa Sinari na Arioki mufalme wa Elasari: wafalme wane kupigana na wafalme watano. Bonde la Sidimu lilikuwa limejaa mashimo ya kabulimbo; kwa hiyo wafalme wa Sodoma na Gomora walipokuwa wakikimbia vita, wakatumbukia mule, lakini wengine wakatorokea kwenye mulima. Basi, wale walioshinda, wakanyanganya mali yote ya Sodoma na Gomora, hata na mazao yao, wakajiendea. Wakamukamata hata Loti mwana wa ndugu ya Abramu aliyekuwa anakaa Sodoma, pamoja na mali yake, wakajiendea. Mutu mumoja aliyeponyoka, akakwenda kumwarifu Abramu Mwebrania ambaye alikuwa anaishi karibu na mielo ya Mamure Mwamori. Mamure alikuwa ndugu ya Eskoli na Aneri. Wote walikuwa wamefanya agano na Abramu. Abramu alipopata habari kwamba mwipwa wake amekamatwa kuwa mufungwa, akatoka na watu wake mashujaa mia tatu na kumi na wanane waliozaliwa katika nyumba yake, akawafuatilia waadui mpaka Dani. Kule, akagawanya jeshi lake katika makundi. Usiku, akawashambulia waadui zake, akawashinda na kuwafukuza mpaka Hoba, upande wa kaskazini wa Damasiki. Basi, Abramu akakomboa mali yote iliyonyanganywa na waadui, na kumukomboa mwipwa wake Loti, mali yake, pamoja na wanawake na watu wengine. Abramu aliporudi kisha kumushinda mufalme Kedorilaomeri na wenzake, mufalme wa Sodoma akatoka na kwenda kukutana naye katika bonde la Sawe ni kusema bonde la Mufalme. Naye Melkisedeki, mufalme wa muji wa Salemu, ambaye alikuwa kuhani wa Mungu Mukubwa, akaleta mukate na divai, akamubariki Abramu akisema: “Abramu abarikiwe na Mungu Mukubwa, Muumba wa mbingu na dunia! Atukuzwe Mungu Mukubwa, aliyetia waadui zako katika mikono yako!” Naye Abramu akamupa Melkisedeki sehemu moja ya kumi ya vitu vyote alivyokuwa navyo. Mufalme wa Sodoma akamwambia Abramu: “Unipe wale watu, lakini ujitwalie mali yote wewe mwenyewe.” Lakini Abramu akamwambia mufalme wa Sodoma: “Ninaapa kwa Yawe, Mungu Mukubwa, aliyeumba mbingu na dunia, kwamba sitatwaa uzi au kamba ya kiatu, wala chochote kinachokuwa chako, kusudi usijivune na kusema kwamba umenitajirisha. Basi, sitatwaa kitu chochote isipokuwa tu vile vitu ambayo vijana wangu walikula na sehemu ya wale waliokuwa pamoja nami – Aneri, Eskoli na Mamure – ambao wana haki nayo.” Nyuma ya mambo hayo, neno la Yawe lilimufikia Abramu katika maono kusema hivi: “Abramu! Usiogope! Mimi ni ngao yako. Zawadi yako itakuwa kubwa!” Lakini Abramu akasema: “Ee Yawe, utanipa nini wakati ninaendelea kuishi bila mutoto, na murizi wangu ni Eliezeri wa Damasiki? Angalia, haujanijalia mutoto. Mutumwa aliyezaliwa ndani ya nyumba yangu ndiye atakayekuwa murizi wangu!” Halafu neno la Yawe lilimufikia kusema hivi: “Huyu hatakuwa murizi wako! Mwana wako atakayetoka katika tumbo lako ndiye atakayekuwa murizi wako.” Yawe akamupeleka Abramu inje na kumwambia: “Angalia mbinguni! Uhesabu nyota, kama kweli utaweza kuzihesabu! Hivi ndivyo wazao wako watakavyokuwa wengi!” Abramu alimwamini Yawe, naye Yawe akamuhesabu kuwa mwenye haki. Yawe akamwambia Abramu: “Mimi ni Yawe niliyekuleta toka Uri, muji wa Wakaldea, kusudi nikupe inchi hii uirizi.” Lakini Abramu akamwambia: “Ee Yawe, nitajua namna gani kwamba nitarizi inchi hii?” Yawe akamwambia: “Uniletee ngombe dike wa miaka mitatu, mwana-mbuzi dike wa miaka mitatu, kondoo dume wa miaka mitatu, na hua na kitoto cha njiwa.” Abramu akamuletea hao wote, akakata kila nyama vipande viwili, akavipanga katika mistari miwili, vikielekeana. Lakini ndege hakuwakata vipande viwili. Na tai waliposhuka juu ya mizoga hiyo, Abramu akakuwa anawafukuza. Jua lilipokuwa likitua, Abramu akashikwa na usingizi muzito. Hofu na giza nene vikamufunika. Yawe akamwambia Abramu: “Ujue hakika kwamba wazao wako watakaa kama wageni katika inchi isiyokuwa yao, watakuwa watumwa na watateswa kwa muda wa miaka mia ine. Hata hivyo, nitaazibu taifa watakalotumikia na kwa mwisho watatoka wakiwa na mali nyingi. Lakini wewe mwenyewe utaishi maisha marefu na kufa kwa amani. Wazao wako watarudi hapa katika kizazi cha ine, kwa sababu uovu wa Waamori haujakamilika bado.” Jua lilipokwisha kutua na giza kuingia, furu inayofuka moshi na mwenge unaowaka moto vikapita katikati ya vile vipande vya nyama. Siku hiyo, Yawe akafanya agano na Abramu akisema: “Ninawapa wazao wako inchi hii, toka muto Nili wa Misri mpaka ule muto mukubwa wa Furati, ni kusema inchi za Wakeni, Wakenizi, Wakadimoni, Wahiti, Waperizi, Warefaimu, Waamori, Wakanana, Wagirgasi na Wayebusi.” Basi, Sarai, muke wa Abramu, alikuwa bado hajamuzalia mutoto, naye alikuwa na mujakazi aliyeitwa Hagari, kutoka Misri. Basi, Sarai akamwambia Abramu: “Unajua kwamba Yawe hajanijalia kupata watoto. Umutwae Hagari mujakazi wangu. Labda nitapata watoto kutoka kwake.” Abramu akakubali shauri la Sarai. Kisha, Sarai akamupa Abramu Hagari, mujakazi wake Mumisri, akuwe muke wake. Haya yalitokea nyuma ya Abramu kukaa katika inchi ya Kanana kwa muda wa miaka kumi. Abramu akatwaa Hagari, naye Hagari akapata mimba. Lakini mara tu alipoona amepata mimba, Hagari akaanza kumuzarau bibi mukubwa wake. Sarai akamwambia Abramu: “Lazima ya ubaya ninaotendewa ikuwe juu yako. Mimi nilikupa mujakazi wangu, lakini alipopata mimba, mimi nimekuwa kitu bure mbele ya macho yake! Yawe ahukumu kati yako na mimi!” Lakini Abramu akamwambia Sarai: “Mujakazi wako yuko chini ya mamlaka yako. Umutendee jinsi unavyopenda.” Basi, Sarai akamutesa Hagari mpaka akatoroka. Malaika wa Yawe akamukuta Hagari kwenye chemichemi ya maji katika jangwa, chemichemi iliyokuwa katika njia kuelekea Suri. Malaika akamwuliza: “Hagari, mujakazi wa Sarai! Unatoka wapi na unakwenda wapi?” Hagari akamujibu: “Ninamukimbia bibi mukubwa wangu Sarai.” Yule malaika wa Yawe akamwambia: “Rudi kwa bibi mukubwa wako Sarai na umutii.” Zaidi ya hayo, malaika wa Yawe akamwambia Hagari: “Nitawazidisha wazao wako hata wasiweze kuhesabika kwa wingi wao.” Kisha huyo malaika wa Yawe akamwambia: “Wewe una mimba na utazaa mutoto mwanaume; utamwita Isimaeli, maana Yawe ameyaona mateso yako. Isimaeli ataishi kama punda wa pori. Atapigana na kila mutu na kila mutu atapigana naye. Ataishi peke yake, akijitenga na watu wa jamaa yake.” Basi, Hagari akamupa Yawe aliyezungumuza naye kule jina la “Wewe ni Mungu Anayeona,” kwa maana alifikiri: “Kweli hapa nimemwona yeye anayeniona?” Ndiyo maana kile kisima kinaitwa “Kisima cha yule anayeishi na anayeniona”. Kisima hiki kipo kati ya Kadesi na Beredi. Hagari akamuzalia Abramu mutoto mwanaume. Abramu akamwita mutoto huyo Isimaeli. Abramu alikuwa na umri wa miaka makumi nane na sita wakati Hagari alipozaa Isimaeli. Wakati Abramu alipokuwa na umri wa miaka makumi tisa na tisa, Yawe akamutokea, akamwambia: “Mimi ni Mungu Mwenye Uwezo. Uendelee mbele yangu na kuwa mukamilifu. Nami nitafanya agano nawe na kuwazidisha wazao wako.” Abramu akaanguka uso mpaka chini. Naye Mungu akamwambia: “Ninafanya agano hili nawe: Utakuwa baba ya mataifa mengi. Tangu sasa, hautaitwa tena Abramu, lakini utaitwa Abrahamu, maana nimekufanya kuwa baba ya mataifa mengi. Nitakufanya ukuwe na wazao wengi sana. Toka kwako nitatokeza mataifa mengi na wafalme. “Nitasimamisha agano langu nawe, wazao wako na vizazi vyao vyote milele; nitakuwa Mungu wako na Mungu wa wazao wako milele. Nitakupa wewe na wazao wako inchi hii ambamo unaishi kama mugeni. Ni kusema inchi yote ya Kanana ikuwe mali yenu milele; nami nitakuwa Mungu wao.” Kisha Mungu akamwambia Abrahamu: “Kwa upande wako, wewe utalishika agano langu, wewe peke yako, wazao wako na vizazi vyao vyote. Hivi ndivyo munavyopaswa kufanya wewe na wazao wako: kila mwanaume kati yenu anapaswa kutahiriwa. Mutatahiriwa kwa kukata magovi yenu na hiki kitakuwa ndicho kitambulisho cha agano kati yangu nanyi. Mwanaume yeyote asiyetahiriwa atatengwa na watu, maana atakuwa amevunja agano langu.” Kisha Mungu akamwambia Abrahamu: “Kuelekea muke wako, hautamwita tena jina lake Sarai, lakini jina lake litakuwa Sara. Nitamubariki, naye atakuzalia mutoto mwanaume. Nitamubariki Sara, naye atakuwa mama wa mataifa mengi na wafalme wa mataifa watatoka kwake.” Hapo Abrahamu akainama uso mpaka chini, akacheka ndani ya moyo wake akiwaza: “Itawezekana kweli mutoto kuzaliwa kwa muzee wa miaka mia moja? Na namna gani, Sara ambaye umri wake ni miaka makumi tisa, ataweza kupata mutoto?” Basi, Abrahamu akamwambia Mungu: “Ingekuwa heri ukubali ahadi hiyo yako imwelekee Isimaeli.” Mungu akamujibu: “Hapana. Muke wako Sara atakuzalia mutoto mwanaume, nawe utamwita Isaka. Nitaimarisha agano langu kwake na wazao wake, kuwa agano la milele. “Na juu ya Isimaeli, nimesikia ombi lako. Nitamubariki, nitamujalia watoto wengi na kuwazidisha sana. Isimaeli atakuwa baba wa watawala kumi na wawili, nami nitamufanya kuwa baba wa taifa kubwa. Lakini agano langu litasimama kwa Isaka ambaye Sara atakuzalia katika mwaka kwa wakati kama huu.” Basi, Mungu alipomaliza kuongea, akamwacha Abrahamu. Kisha Abrahamu akamutahiri mwana wake Isimaeli, na kuwatahiri watumwa wanaume wote waliozaliwa katika nyumba yake na walionunuliwa kwa feza zake. Aliwatahiri wote siku hiyohiyo kama vile Mungu alivyomwamuru. Abrahamu alikuwa na umri wa miaka makumi tisa na tisa alipotahiriwa. Na Isimaeli mwana wake alikuwa na umri wa miaka kumi na mitatu alipotahiriwa. Abrahamu na mwana wake Isimaeli pamoja na wanaume wote wa nyumba yake, watumwa wote waliozaliwa katika nyumba yake na wote walionunuliwa kwa feza zake walitahiriwa siku hiyohiyo. Yawe alimutokea Abrahamu kwenye miti ya mielo ya Mamure. Abrahamu alikuwa anaikaa kwenye mulango wa hema yake wakati wa joto la muchana. Alipoinua macho yake, akaona watu watatu wakisimama mbali kidogo mbele yake. Mara tu alipowaona, akakimbia kutoka kwenye mulango wa hema yake, akakwenda kuwapokea. Alipowafikia akainama kwa heshima na kusema: “Bwana wangu, nikipata kukubaliwa mbele yako, tafazali usinipite mimi mutumishi wako lakini ushinde kwangu. Mutaletewa maji kidogo kusudi munawe miguu na kupumzika chini ya muti. Wakati munapopumzika, nitatayarisha chakula kidogo mukule, kusudi mupate nguvu za kuendelea na safari yenu; maana mumenifikia mimi mutumishi wenu.” Nao wakasema: “Sawa! Fanya kama ulivyosema.” Abrahamu akarudi haraka ndani ya hema akamwambia Sara: “Tayarisha haraka vipimo vitatu vya unga bora, uuponde, uchome mikate.” Kisha akatoka haraka akakwenda kwenye kundi la ngombe, akachagua mwana-ngombe mumoja muzuri na munono, akamupatia mutumishi ambaye aliharakisha kumuchinja na kumupika. Halafu Abrahamu akachukua siagi, maziwa na ile nyama uliotayarishwa, akawatayarishia wageni hao chakula; naye akasimama karibu nao walipokuwa wakikula chini ya muti. Wale wageni wakamwuliza: “Muke wako Sara yuko wapi?” Abrahamu akawajibu: “Yuko ndani ya hema.” Mumoja wao akasema: “Hakika nitakurudilia kwa wakati kama huu katika mwaka na muke wako Sara atakuwa na mutoto mwanaume.” Sara alikuwa kule nyuma kwenye mulango wa hema, akisikiliza. Abrahamu na Sara walikuwa wazee sana, naye Sara hangeweza tena kuzaa. Kwa hiyo, Sara alicheka kimoyomoyo akisema: “Mimi ni muzee, na mume wangu vilevile. Basi, nikiwa muzee hivi, nitaweza kufurahi na kupata watoto?” Kwa hiyo Yawe akamwuliza Abrahamu: “Kwa nini Sara amecheka na kujiuliza kama kweli itawezekana apate mutoto akiwa muzee? Kuna jambo lolote lisilowezekana kwa Yawe? Nitakurudilia wakati uliopangwa, kwa wakati kama huu katika mwaka, na Sara atakuwa na mutoto mwanaume.” Lakini Sara, akiwa na hofu, akakana akisema: “Sikucheka!” Yawe akamwambia: “Ndiyo, ulicheka!” Kisha wale watu wakaondoka, wakafika pahali walipoweza kuona muji wa Sodoma; naye Abrahamu akawasindikiza. Basi, Yawe akawaza: “Nimufiche Abrahamu jambo ambalo nimepanga kutenda? Yeye atakuwa baba wa taifa kubwa na kwa njia yake mataifa yote ya ulimwengu yatabarikiwa! Nimemuchagua yeye na wazao wake. Yeye atawafundisha wazao wake kushika njia yangu kwa kutenda kwa haki na kwa kufuata sheria yangu, nami nitawatimizia ahadi zangu.” Basi, Yawe akasema: “Kuna malalamiko mengi juu ya watu wa Sodoma na Gomora, na zambi yao ni kubwa sana. Hivyo nitashuka kwenda kule nijionee mwenyewe kama kweli wamefanya kadiri ya kilio kilichonifikia. Ninataka kujua.” Kutoka pale, wale watu wakashika njia kuelekea Sodoma, lakini Yawe akabaki, akisimama pamoja na Abrahamu. Basi, Abrahamu akamukaribia Yawe, akamwuliza: “Ni kweli utawaangamiza watu wa haki pamoja na waovu? Labda kuna watu wa haki makumi tano katika muji. Utauangamiza muji muzima kuliko kuuacha kwa sababu ya wale wa haki makumi tano wanaokuwa mule? Sizani kama utafanya hivyo, kuwaua watu wa haki pamoja na waovu, kutendea watu wa haki sawa na waovu. Hapana, haiwezekani! Mwamuzi wa dunia yote hataacha kutenda mambo yanayokuwa sawa!” Yawe akamwambia: “Nikikuta watu wa haki makumi tano kule katika muji wa Sodoma, basi nitaacha muji wote salama kwa ajili yao.” Abrahamu akasema: “Nimesubutu kuzungumuza na Bwana, mimi ninayekuwa mavumbi na majivu tu. Labda kutapatikana watu wa haki makumi ine na watano pahali pa makumi tano. Utaangamiza muji muzima kwa sababu kumepunguka watu watano?” Yawe akamujibu: “Sitaangamiza muji ikiwa kuna watu wema makumi ine na watano.” Abrahamu akaongeza kusema: “Pengine watu makumi ine watapatikana mule.” Yawe akamujibu: “Kwa ajili ya watu wema makumi ine, sitafanya hivyo.” Abrahamu akaongeza kusema: “Ee Bwana, ninaomba usinikasirikie, nami nitasema tena. Labda kutapatikana watu wema makumi tatu.” Yawe akamujibu: “Sitafanya hivyo nikiwakuta hao makumi tatu.” Abrahamu akasema: “Nimesubutu kuzungumuza na Bwana. Labda kutapatikana watu wema makumi mbili.” Yawe akamujibu: “Kwa ajili ya hao makumi mbili, sitauangamiza.” Kisha Abrahamu akasema: “Ee Bwana, ninakuomba usikasirike, lakini nitasema tena mara moja tu. Labda kutapatikana watu wema kumi.” Yawe akamujibu: “Kwa ajili ya hao watu wema kumi, sitaangamiza muji ule.” Yawe alipomaliza kuzungumuza na Abrahamu, akajiendea naye Abrahamu akarudi kwake. Wale wamalaika wawili wakafika katika muji wa Sodoma magaribi. Loti alikuwa ameketi kwenye mulango wa muji wa Sodoma. Alipowaona, akasimama kwenda kuwapokea, akainama kwa heshima. Akasema: “Bwana zangu, karibu katika nyumba yangu mimi mutumishi wenu. Munaweza kunawa miguu na kulala kwangu usiku wa leo. Asubui mapema mutaweza kuendelea na safari yenu.” Lakini, wao wakasema: “Hapana! Sisi tutalala huku katika barabara.” Loti akawasihi sana, kwa mwisho wakakubali, wakageuka na kuingia katika nyumba yake. Loti akatayarisha karamu, akachoma mikate isiyotiwa chachu, wakakula. Lakini mbele ya kulala usiku, wanaume wote wa muji wa Sodoma, vijana na wazee, bila kubaki hata mumoja, wakazunguka nyumba ya Loti. Wakamwita Loti na kumwuliza: “Wako wapi wale wanaume waliokuja kwako? Uwatoshe inje. Tunataka kulala nao.” Loti akatoka inje, akafunga mulango nyuma yake, akawaambia: “Wandugu zangu, ninawasihi musitende uovu ule. Angalia, nina wabinti wawili ambao bado hawajalala na mwanaume. Muniruhusu niwape hao wabinti muwatendee kama vile munavyopenda. Lakini musiwatendee lolote wanaume hawa kwa sababu ni wageni wangu.” Lakini wao wakasema: “Utupitishe! Wewe ulikuja huku ukiwa mugeni na sasa unajifanya kuwa mwamuzi! Basi, tutakutendea mabaya zaidi ya wale wageni wako.” Halafu wakamusukuma Loti nyuma hata karibu wavunje mulango wake. Lakini wale wageni wakanyoosha mikono yao, wakamukokotea Loti ndani ya nyumba na kufunga mulango. Kisha wakawapiga kwa kuwapofusha macho wanaume wote waliokuwa kwa mulango, wakubwa na wadogo, hata wakataabika kwa kutafuta ule mulango, nao hawakuupata. Wale watu wawili wakamwambia Loti: “Uko na mutu mwingine hapa, pengine wana wako, wabinti, wachumba wa wabinti zako au watu wengine wa jamaa yako wanaoishi katika muji huu? Uwatoshe pahali hapa haraka, kwa maana kilio kilichomufikia Yawe juu ya wakaaji wa hapa ni kikubwa sana, naye ametutuma tukuje kuwaangamiza.” Basi, Loti akawaendea wachumba wa wabinti zake, akawaambia: “Haraka! Mutoke pahali hapa, maana Yawe atauangamiza muji huu.” Lakini wao wakamwona kama mutu mwenye kuchekesha tu. Kulipokucha, wamalaika wakamusihi Loti wakisema: “Amuka, utwae muke wako na hawa wabinti zako wawili musipate kuangamia wakati muji huu unapoazibiwa.” Loti akakuwa anasitasita. Lakini kwa vile Yawe alivyomuhurumia Loti, wale wamalaika wakamushika yeye, muke wake na wabinti zake wawili, wakamutosha inje ya muji. Walipowatosha inje ya muji, malaika mumoja wao akawaambia: “Mukimbie kwa ajili ya usalama wenu. Musiangalie nyuma wala kusimama popote katika bonde. Mukimbilie kwenye milima, musipate kuangamia.” Loti akamwambia: “Hapana vile, ee bwana wangu! Ni kweli kwamba mimi mutumishi wako nimepata kukubaliwa mbele yako, nawe umenitendea mema sana kwa kuokoa maisha yangu. Lakini kwenye milima ni mbali sana. Maangamizi haya yatanikuta mbele sijafika kule, nami nitakufa. Tafazali, kule kuna muji mudogo ambao ninaweza kukimbilia maana uko karibu. Basi, uniruhusu nikimbilie kule. Ule ni muji mudogo tu, na kule nitaponyoka.” Naye akamujibu: “Sawa, nimekubali ombi lako. Sitaangamiza muji uliotaja. Harakisha! Kimbilia kule, nami sitafanya lolote mpaka utakapofika kule.” Hivyo muji ule ukaitwa Soari. Jua lilikuwa limekwisha kupanda juu wakati Loti alipofika katika muji wa Soari. Halafu Yawe akateremusha moto mukali wa kiberiti kutoka mbinguni juu ya Sodoma na Gomora, akaiangamiza miji hiyo, bonde lote, wakaaji wake wote na mimea yote katika inchi hiyo. Lakini muke wa Loti aliyekuwa nyuma ya Loti, akatazama nyuma, akageuka nguzo ya chumvi. Asubui mapema, Abrahamu alikwenda pahali alipokuwa akisimama mbele ya Yawe. Akiwa pale, akatazama chini pande za Sodoma na Gomora na eneo lote la bonde, akashangaa kuona moshi ukipanda, moshi kama wa furu kubwa. Mungu alipoangamiza miji katika bonde ambamo Loti alikuwa anakaa, alimukumbuka Abrahamu kwa kumutosha Loti katika miji hiyo, kusudi Loti asiangamizwe pamoja nayo. Loti aliogopa kuishi katika muji wa Soari, kwa hiyo akahama toka muji ule, yeye pamoja na wabinti zake wawili, wakakwenda kuishi ndani ya pango kwenye milima. Wakiwa kule, binti mukubwa akamwambia dada yake: “Baba yetu ni muzee na hakuna mwanaume katika inchi wa kutuoa tupate watoto. Basi, tumuleweshe baba kwa divai, kusudi tupate kulala naye na kudumisha uzao kwa kupata watoto kwa njia yake.” Usiku ule wakamulewesha baba yao kwa divai. Yule binti wa kwanza akakwenda akalala naye. Lakini baba yake hakujua wakati binti yake alipolala naye, wala wakati alipoondoka. Kesho yake, yule binti wa kwanza akamwambia yule mudogo: “Jana usiku mimi nililala na baba. Leo vilevile tumuleweshe kwa divai, kisha wewe utalala naye, na hivyo sisi wote tutadumisha uzao kwa kupata watoto.” Basi, usiku ule vilevile wakamulewesha baba yao kwa divai, kisha yule binti mudogo akakwenda akalala naye. Lakini baba yake hakujua wakati binti yake alipolala naye, wala wakati alipoondoka. Hivyo, wabinti wote wawili za Loti wakapata mimba kutokana na baba yao. Yule binti wa kwanza akazaa mutoto mwanaume, akamwita Moabu. Huyo ndiye baba wa Wamoabu mpaka leo. Yule mudogo vilevile akazaa mutoto mwanaume, akamwita Beni-Ami. Huyo ndiye baba wa Waamoni mpaka leo. Abrahamu alisafiri toka kule na kuelekea eneo la Negebu, akafanya makao yake kati ya Kadesi na Suri, kisha akakwenda kukaa kwa muda kule Gerari. Akiwa kule, Abrahamu alisema kwamba muke wake Sara ni dada yake. Kwa hiyo, mufalme Abimeleki wa Gerari akamutwaa Sara. Lakini Mungu akamufikia Abimeleki katika ndoto usiku, akamwambia: “Wewe utakufa kwa sababu ya mwanamuke uliyemutwaa, maana yuko na mume wake.” Abimeleki ambaye bado hakukuwa amelala na Sara, akajibu: “Bwana, utawaua watu wasiokuwa na kosa? Si ni Abrahamu mwenyewe ndiye aliyesema kwamba huyu ni dada yake? Tena hata Sara mwenyewe alisema kwamba Abrahamu ni kaka yake! Mimi nimefanya nilivyofanya kwa moyo safi na sina kosa.” Basi, Mungu akamwambia katika hiyo ndoto: “Sawa. Ninajua kwamba umefanya hivyo kwa moyo safi. Mimi ndiye niliyekuzuia kutenda zambi mbele yangu. Ndiyo maana sikukuruhusu umuguse huyo mwanamuke. Sasa umurudishe yule mwanamuke kwa mume wake. Abrahamu ni nabii. Atakuombea nawe utaishi. Lakini usipomurudisha, ujue kwa hakika kwamba wewe utakufa pamoja na watu wako wote.” Basi, Abimeleki akaamuka asubui mapema, akawaita watumishi wake wote na kuwaelezea mambo aliyoona katika ndoto. Nao wakaogopa sana. Kwa hiyo Abimeleki akamwita Abrahamu, akamwuliza: “Umetutendea nini? Nimekukosea nini hata ukaniletea zambi kubwa, mimi na ufalme wangu? Umenitendea mambo yasiyostahili kutendwa.” Tena Abimeleki akazidi kumwuliza: “Ni kitu gani kimekusukuma kufanya hivyo?” Abrahamu akamujibu: “Nilifanya hivyo kwa sababu hakuna anayemwogopa Mungu pahali hapa na kwamba mungeniua kusudi mumutwae muke wangu. Zaidi ya hayo, kwa kweli, yeye ni dada yangu: baba yake na baba yangu ni mumoja, lakini mama tofauti; ndiyo maana aliweza kuwa muke wangu. Wakati Mungu aliponifanya niache nyumba ya baba yangu na kwenda kutangatanga, nilimwambia muke wangu: ‘Popote tutakapokwenda, tafazali useme kwamba mimi ni kaka yako!’ ” Abimeleki akamurudishia Abrahamu muke wake Sara, akamupa kondoo, ngombe na watumwa na wajakazi. Tena Abimeleki akamwambia Abrahamu: “Angalia, inchi hii yote ni yangu! Basi, chagua popote unapopenda, ukae.” Kisha, akamwambia Sara: “Mimi nimemupa ndugu yako vikoroti elfu moja vya feza kwa kuwaonyesha wote wanaokuwa pamoja nawe kwamba hauna kosa. Umehakikishwa kwamba hauna kosa.” Kisha Abrahamu akamwomba Mungu, naye akamuponyesha Abimeleki, muke wake na wajakazi wake, hata wakaweza kupata tena watoto. Hapo mbele Yawe alikuwa amewazuia wanawake wote wa nyumba ya Abimeleki kupata watoto kwa sababu ya Sara, muke wa Abrahamu. Yawe akamukumbuka Sara, akamutendea kama alivyoahidi. Basi, Abrahamu akiwa muzee, Sara akapata mimba, akamuzalia mutoto mwanaume, wakati uleule Mungu aliotaja. Abrahamu akamupa huyo mwana wake ambaye Sara alimuzalia jina la Isaka. Isaka alipotimiza umri wa siku nane, Abrahamu akamutahiri kama alivyoamuriwa na Mungu. Abrahamu alikuwa na umri wa miaka mia moja wakati mwana wake Isaka alipozaliwa. Naye Sara akasema: “Mungu amenipatia kicheko; yeyote atakayesikia habari hizi, atacheka pamoja nami.” Kisha akaongeza: “Ni nani angeweza kumwambia Abrahamu kwamba mimi Sara nitanyonyesha watoto? Tena nimemuzalia mutoto mwanaume katika uzee wake!” Isaka akaendelea kukomaa, na siku alipoachishwa kunyonya, Abrahamu akafanya karamu kubwa. Siku moja Sara akamwona Isimaeli, mutoto wa Abrahamu aliyezaliwa na Hagari Mumisri, akicheza na Isaka mwana wake. Basi, Sara akamwambia Abrahamu: “Fukuza mujakazi huyu na mwana wake. Haiwezekani kabisa mutoto wa mujakazi kurizi pamoja na mwana wangu Isaka.” Jambo hili lilimuhuzunisha sana Abrahamu kwa sababu Isimaeli vilevile alikuwa mutoto wake. Lakini Mungu akamwambia Abrahamu: “Usihuzunike kwa sababu ya mutoto huyu, wala huyo mujakazi wako. Jambo lolote Sara atakalokuambia ulifanye. Maana ni kwa njia ya Isaka utapata wazao watakaoitwa wako. Na juu ya huyo mwana wa mujakazi wako nitamufanya akuwe baba wa taifa kubwa kwa sababu yeye vilevile ni mutoto wako.” Hivyo, asubui mapema, Abrahamu akatwaa chakula na chupa la maji, akamupa Hagari na kumubebesha mutoto juu ya bega. Akamufukuza pamoja na mwana wake. Hagari akaondoka, akakuwa anatangatanga katika jangwa la Beri-Seba. Wakati maji yalipomwishia katika lile chupa, Hagari akamulalisha mwana wake chini ya muti. Naye akakwenda kando, akaikaa umbali wa kama metre mia moja hivi, akisema ndani ya moyo wake: “Heri nisimwone mwana wangu akikufa.” Na alipokuwa amekaa pale, mutoto akalia kwa sauti kubwa. Mungu akamusikia mutoto yule akilia, na malaika wa Mungu akamwita Hagari kutoka mbinguni, akamwambia: “Una shida gani Hagari? Usiogope. Mungu amesikia sauti ya mutoto kule anapokuwa. Simama umwinue mutoto na kumushika vizuri katika mikono yako, maana nitamufanya akuwe baba wa taifa kubwa.” Mungu akamufumbua Hagari macho, naye akaona kisima cha maji. Akakwenda akajaza chupa maji, akamukunywesha mutoto wake. Mungu akakuwa pamoja na yule mutoto, naye akaendelea kukomaa. Alikaa katika jangwa na akakuwa mupiga upinde hodari sana. Alikuwa akikaa katika jangwa za Parani, na mama yake akamwoea muke kutoka inchi ya Misri. Wakati ule, Abimeleki pamoja na Fikoli, jemadari wa jeshi lake, akamwendea Abrahamu, akamwambia: “Mungu yuko pamoja nawe katika kila kitu unachofanya. Kwa hiyo uniapie kwa jina la Mungu kwamba hautanidanganya mimi au watoto wangu au wazao wangu. Kadiri mimi nilivyokutendea mema, vivyo hivyo nawe unitendee mema mimi na inchi hii unamokaa.” Abrahamu akasema: “Ninaapa.” Wakati ule Abrahamu alikuwa amemwonya Abimeleki juu ya kisima cha maji ambacho watumishi wa Abimeleki walikuwa wamemunyanganya. Abimeleki akamwambia: “Mimi sijui nani aliyefanya hivyo. Mpaka leo hii wewe haukuniambia, wala mimi sijapata kusikia habari hizi mpaka leo.” Basi, Abrahamu akatwaa kondoo na ngombe akamupa Abimeleki nao wawili wakafanya agano kati yao. Abrahamu akatenga wana-kondoo dike saba. Abimeleki akamwuliza Abrahamu: “Kwa nini unawatenga hao wana-kondoo dike saba?” Abrahamu akamujibu: “Hawa wana-kondoo dike saba ninakupa kwa mukono wangu mwenyewe kama ushuhuda wangu kwamba mimi ndiye niliyechimba kisima hiki.” Kwa hiyo kisima hicho kikaitwa Beri-Seba, maana wote wawili walifanya kiapo pahali pale. Hivyo, wakafanya agano kule Beri-Seba. Abimeleki na Fikoli, jemadari wa jeshi lake, akaondoka na kurudi katika inchi ya Wafilistini. Abrahamu akapanda muti wa mukwaju kule Beri-Seba, akaomba kwa jina la Yawe, akamwabudu Mungu, Mungu wa milele. Abrahamu alikaa katika inchi ya Wafilistini muda murefu. Nyuma ya mambo yale, Mungu alimupima Abrahamu. Mungu alimwita: “Abrahamu!” Naye akaitika: “Niko hapa.” Mungu akamwambia: “Umutwae mwana wako, Isaka, mwana wako wa pekee unayemupenda, uende mpaka inchi ya Moria, umutoe kuwa sadaka ya kuteketezwa kwa moto juu ya mulima nitakaokuonyesha.” Basi, kesho yake, Abrahamu akaamuka asubui mapema, akatandika punda wake, akawatwaa watumishi wake wawili pamoja na Isaka mwana wake. Akatayarisha kuni kwa ajili ya sadaka ya kuteketezwa kwa moto, kisha akaanza safari kuelekea pahali alipoambiwa na Mungu. Kwa siku ya tatu, Abrahamu aliinua macho akaona pahali pale kwa mbali. Akawaambia wale watumishi wake: “Mungoje hapa na huyu punda. Mimi na mwana wangu tutakwenda mpaka kule, tutamwabudu Mungu, kisha tutawarudilia.” Basi, Abrahamu akatwaa zile kuni, akamubebesha Isaka mwana wake. Yeye mwenyewe akatwaa moto na kisu katika mukono, wakaondoka pamoja. Isaka akamwuliza baba yake: “Baba, tuko na moto na kuni. Lakini mwana-kondoo wa sadaka ya kuteketezwa yuko wapi?” Abrahamu akamujibu: “Mwana wangu, Mungu mwenyewe atatujalia mwana-kondoo wa sadaka ya kuteketezwa.” Basi, wakaendelea na safari yao. Walipofika pahali ambapo Mungu alipomwagiza, Abrahamu akajenga mazabahu na kupanga kuni juu yake. Kisha akamufunga Isaka mwana wake na kumulalisha juu ya kuni kwenye mazabahu. Abrahamu akanyoosha mukono wake, akatwaa kisu tayari kumuchinja mwana wake. Lakini malaika wa Yawe akamwita kutoka mbinguni: “Abrahamu! Abrahamu!” Naye akaitika: “Niko hapa!” Malaika akamwambia: “Usinyooshe mukono wako juu ya kijana wala usimufanyie jambo lolote! Sasa ninajua kwamba unamwogopa Mungu, maana haukuninyima hata mwana wako wa pekee.” Halafu Abrahamu akainua macho, akaona kondoo dume, amenaswa pembe zake katika kichaka. Basi, akakwenda, akamutwaa yule kondoo, akamutoa sadaka ya kuteketezwa kwa moto pahali pa mwana wake. Kwa hiyo, Abrahamu akapaita pahali pale: “Yawe anajalia,” kama inavyosemwa hata leo: “Kwa mulima wa Yawe, watu wanajaliwa.” Malaika wa Yawe akamwita Abrahamu mara ya pili kutoka mbinguni, akamwambia: “Yawe anasema hivi: Nimeapa kwa nafsi yangu mwenyewe kwamba kwa sababu umefanya hivi, wala haukuninyima mwana wako wa pekee, hakika nitakubariki, na wazao wako nitawazidisha kama nyota mbinguni na kama muchanga pembeni ya bahari. Wazao wako watarizi miji ya waadui zao. Kutokana na wazao wako mataifa yote katika dunia yatabarikiwa kwa sababu wewe umeitii amri yangu.” Basi, Abrahamu akawarudilia wale watumishi wake, nao pamoja wakaondoka, wakarudi Beri-Seba. Abrahamu akakaa kule Beri-Seba. Nyuma ya mambo hayo Abrahamu akapata habari kwamba Milka vilevile amemuzalia ndugu yake Nahori watoto wanaume: Usi muzaliwa wa kwanza, Buzi ndugu yake, Kemweli baba ya Aramu, Kesedi, Hazo, Pildasi, Idilafu na Betueli. Betueli alizaa Rebeka. Milka alimuzalia Nahori, ndugu ya Abrahamu, watoto hao wanane. Zaidi ya hayo, Reuma, habara ya Nahori, vilevile alimuzalia watoto: Teba, Gahamu, Tahasi na Maka. Sara aliishi miaka mia moja makumi mbili na saba. Hiyo ndiyo iliyokuwa miaka ya maisha ya Sara. Alikufia kule Kiriati-Arba, ni kusema Hebroni, katika inchi ya Kanana. Abrahamu akaomboleza na kumufanyia Sara muke wake kilio. Abrahamu akaacha maiti ya muke wake, akatoka na kwenda kuzungumuza na Wahiti, akawaambia: “Mimi ninaishi kama mugeni kati yenu. Munipatie sehemu ya udongo ya kaburi, kusudi nipate kumuzika marehemu muke wangu.” Wahiti wakamujibu: “Ee bwana wetu, usikilize; wewe ni kiongozi mukubwa kati yetu. Umuzike marehemu muke wako katika kaburi lolote utakalojichagulia; hakuna yeyote kati yetu atakayekunyima kaburi lake, wala kukuzuia kumuzika marehemu muke wako.” Kisha Abrahamu akasimama na kuinama kwa heshima mbele ya wanainchi Wahiti, akawaambia: “Ikiwa munaniruhusu nimuzike marehemu muke wangu, tafazali mumwombe Efuroni mwana wa Sohari, kwa ajili yangu, aniuzishie lile pango lake la Makipela linalokuwa kwa mupaka wa shamba lake. Mumusihi aniuzishie nilifanye makaburi yangu. Anipatie kwa bei ya haki hapahapa mbele yenu.” Efuroni mwenyewe alikuwa kati ya Wahiti hao waliokuwa wamekutanika kwenye mulango wa muji. Basi, Efuroni Muhiti, akamujibu Abrahamu mbele ya Wahiti wote pale kwenye mulango: “Hapana bwana. Tafazali unisikilize. Ninakupa shamba lote na pango linalokuwa mule; tena ninakupa mbele ya wanainchi wenzangu. Umuzike mule marehemu muke wako.” Abrahamu akainama tena kwa heshima mbele ya wanainchi, akamwambia Efuroni, wanainchi wote wakisikia: “Ninakuomba, tafazali unisikilize. Nitakulipa bei kamili ya shamba lako, na ninakuomba upokee malipo haya kusudi nipate kumuzika mule marehemu muke wangu.” Efuroni akamujibu Abrahamu: “Bwana, unisikilize. Shamba lenye bei ya vikoroti mia ine tu za feza ni nini kati yako na mimi? Umuzike marehemu muke wako.” Abrahamu akakubaliana na Efuroni, akamupimia kadiri ya feza alizotaja mbele ya Wahiti wote, feza vikoroti mia ine, kadiri ya vipimo vya wachuuzi wa wakati ule. Basi, shamba la Efuroni linalokuwa kule Makipela, upande wa mashariki ya Mamure, pango na miti yote iliyokuwa kule pamoja na eneo zima, likakuwa la Abrahamu mbele ya Wahiti wote waliokutanika kwa mulango wa muji. Nyuma ya hayo, Abrahamu akamuzika Sara muke wake katika pango lile lililokuwa mule katika shamba la Makipela, upande wa mashariki ya Mamure, ni kusema Hebroni, katika inchi ya Kanana. Shamba na pango lililokuwa mule lililohakikishwa na Wahiti likuwe mali ya Abrahamu apate kuzika wafu wake mule. Sasa Abrahamu alikuwa muzee wa miaka mingi, naye Yawe alikuwa amemubariki katika kila hali. Siku moja Abrahamu akamwambia mutumishi wake aliyekuwa muzee kuliko wengine na musimamizi wa mali yake yote: “Weka mukono wako chini ya paja yangu, nami nitakuapisha kwa jina la Yawe, Mungu wa mbingu na dunia, kwamba hautamwoea mwana wangu binti yeyote kati ya wabinti za Wakanana ninaoishi nao. Uniapie kwamba utakwenda mpaka katika inchi yangu, kwa jamaa zangu, umutafutie mwana wangu Isaka muke.” Mutumishi akamwambia: “Labda mwanamuke yule atakataa kunifuata kuja huku, ikiwa hivyo, ni lazima nimurudishe mwana wako katika inchi ulikotoka?” Abrahamu akamwambia: “Hapana! Angalia sana usimurudishe mwana wangu kule. Yawe, Mungu wa mbingu, aliyenitoa katika nyumba ya baba yangu na kutoka katika inchi nilimozaliwa, na ambaye alisema nami, aliniapia kwamba atawapa wazao wangu inchi hii. Yeye atamutuma malaika wake mbele yako kusudi umuletee mwana wangu muke kutoka kule. Ikiwa mwanamuke yule hatapenda kukufuata mpaka huku, basi kiapo changu hakitakufunga, lakini kwa vyovyote vile usimurudishe mwana wangu kule.” Basi, mutumishi yule akaweka mukono wake chini ya paja la Abrahamu, bwana wake, akaapa juu ya jambo hilo. Kisha, yule mutumishi akatwaa ngamia kumi wa bwana wake akaondoka akiwa na zawadi nzuri za kila aina. Akasafiri kwenda katika muji Nahori alimokaa, katika inchi ya Mesopotamia. Alipofika, alipigisha ngamia wake magoti kando ya kisima kilichokuwa inje ya muji. Ilikuwa magaribi wakati ambapo wanawake wanakwenda kwenye kisima kuteka maji. Naye akaomba: “Ee Yawe, Mungu wa bwana wangu Abrahamu, ninakuomba unisaidie leo na umutendee mema bwana wangu Abrahamu. Niko hapa kando ya kisima ambapo wabinti za wenyeji wa muji wanakuja kuteka maji. Basi, binti nitakayemwambia atue mutungi wake wa maji anipatie maji nikunywe, naye akinipa mimi na kuwakunywesha ngamia wangu, akuwe ndiye uliyemuchagulia mutumishi wako Isaka. Jambo hilo litanionyesha kwamba umemutendea mema bwana wangu.” Mbele hajamaliza kuomba, mara moja Rebeka, binti ya Betueli mwana wa Milka, muke wa Nahori, ndugu ya Abrahamu, akafika akibeba mutungi wake kwenye bega. Binti yule alikuwa na sura ya kuvutia sana na alikuwa angali bikira. Basi, akateremuka kwenye kisima, akaujaza mutungi wake maji na kupanda. Halafu yule mutumishi akaharakisha kukutana naye, akamwambia: “Tafazali, unipatie maji ya kunywa kutoka mutungi wako.” Binti akamujibu: “Kunywa, ee bwana wangu.” Na palepale akatua mutungi wake, akiushikilia kusudi amukunyweshe. Alipokwisha kumupatia maji, akamwambia: “Nitatekea ngamia wako maji vilevile, wakunywe mpaka watosheke.” Basi, akafanya haraka, akawamiminia ngamia maji ya mutungi wake katika birika, akakimbia kwenye kisima kuteka maji mengine na kuwakunywesha ngamia wake wote. Yule mutu akakuwa anamwangalia kwa uangalifu bila kusema lolote, apate kufahamu kama Yawe amefanikisha safari yake au sivyo. Ngamia walipotosheka kunywa maji, yule mutu akamupa yule binti pete ya zahabu yenye uzito wa yapata grama sita, na vikomo viwili vya zahabu za grama kumi kila moja. Akamwuliza: “Uniambie tafazali, wewe ni binti ya nani? Kuna nafasi ya kulala katika nyumba ya baba yako?” Rebeka akajibu: “Mimi ni binti ya Betueli mwana wa Milka, muke wa Nahori. Kwetu kuna majani na malisho ya kutosha na pahali pa kulala kwa wageni.” Halafu yule mutu akainamisha kichwa chake, akamwabudu Yawe akisema: “Atukuzwe Yawe, Mungu wa bwana wangu Abrahamu, ambaye hajasahau wema na uaminifu wake kwa bwana wangu. Yawe ameniongoza mimi mwenyewe moja kwa moja mpaka kwa jamaa ya bwana wangu!” Kisha yule binti akakimbia kwenda kuwapa wandugu za mama yake habari. Rebeka alikuwa na kaka yake anayeitwa Labani. Labani akatoka mbio kukutana na yule mutu kwenye kisima. Labani alikuwa ameona ile pete na vikomo kwa mikono ya dada yake na kusikia mambo Rebeka aliyoambiwa na yule mutu. Labani akamukuta yule mutu akisimama karibu na ngamia wake kando ya kisima. Labani akamwambia: “Karibu kwetu wewe uliyebarikiwa na Yawe. Mbona unasimama inje? Mimi mwenyewe nimekwisha tayarisha nyumba na pahali kwa ajili ya hawa ngamia wako!” Basi, mutumishi yule wa Abrahamu akaingia ndani ya nyumba. Labani akafungua ngamia na kuwapatia majani, akamupa yeye na watu wake maji ya kunawa miguu. Basi, wakamutayarishia chakula, lakini yeye akasema: “Sitakula mpaka niseme ninachotaka kusema.” Labani akamwambia: “Basi, sema.” Yule mutu akasema: “Mimi ni mutumishi wa Abrahamu. Yawe amemubariki sana bwana wangu, naye amekuwa mutu mukubwa. Amemupa makundi ya kondoo na nyama wengi, feza na zahabu, watumishi wanaume na wanawake, ngamia na punda! Sara, muke wa bwana wangu katika uzee wake, alimuzalia bwana wangu mutoto; na bwana wangu amemupa yule mutoto mali yake yote. Bwana wangu aliniapisha mimi akisema: ‘Hautamwoea mwana wangu binti yeyote kati ya wabinti za Wakanana ambao ninaishi katika inchi yao. Lakini utakwenda mpaka katika inchi yangu, kwa jamaa zangu, kusudi umutafutie mwana wangu Isaka muke.’ Nami nikamwambia bwana wangu: ‘Labda mwanamuke yule atakataa kunifuata kuja huku.’ Lakini yeye akasema: ‘Yawe aliyeniongoza katika maisha yangu, atamutuma malaika wake aende pamoja nawe na kukufanikisha katika safari yako. Nawe utamutwalia mwana wangu muke kutoka kwa jamaa yangu na nyumba ya baba yangu. Utakapofika kwa jamaa yangu, nao wasipokupa yule binti, basi, hautafungwa na kiapo changu.’ “Leo nilipofika kwenye kisima nikaomba: ‘Ee Yawe, Mungu wa bwana wangu Abrahamu, ninakuomba unisaidie leo katika safari yangu na umutendee Abrahamu bwana wangu mema. Niko hapa kando ya kisima. Binti atakayekuja kuteka maji ambaye nitamwomba anipatie maji kidogo ya kunywa kutoka mutungi wake, naye akinipa na kuwatekea ngamia wangu maji, basi yule akuwe ndiye uliyemuchagua kuwa muke wa mwana wa bwana wangu.’ “Mbele sijamaliza kuomba ndani ya moyo wangu, mara tu Rebeka akafika na mutungi wake wa maji juu ya bega, akateremuka kwenye kisima na kuteka maji. Nami nikamwambia: ‘Tafazali unipe maji ya kunywa.’ Naye akatua mutungi wake haraka toka juu ya bega lake, akasema: ‘Basi, kunywa bwana wangu. Nitatekea ngamia wako maji vilevile.’ Basi, mimi nikakunywa naye akawapa ngamia wangu maji vilevile. Halafu nilimwuliza: ‘Wewe ni binti ya nani?’ Akaniambia: ‘Mimi ni binti ya Betueli mwana wa Milka, muke wa Nahori.’ Halafu nikamupa pete na kumuvalisha vikomo kwa mikono. Kisha nikainama na kumwabudu Yawe. Nikamutukuza Yawe, Mungu wa bwana wangu Abrahamu, ambaye ameniongoza moja kwa moja kwa binti wa ukoo wa bwana wangu kwa ajili ya mwana wake. Sasa, basi, muniambie kama muko tayari kumutendea bwana wangu kwa wema na uaminifu. Kama sivyo, basi museme, nami nitajua cha kufanya.” Kisha kusikia hayo, Labani na Betueli wakamujibu: “Jambo hili limetoka kwa Yawe, sisi hatuwezi kuamua lolote. Rebeka huyu hapa. Umutwae uende. Akuwe muke wa mwana wa bwana wako kama vile Yawe alivyosema.” Mutumishi wa Abrahamu aliposikia maneno hayo, akamwabudu Yawe. Kisha akatoa vyombo vya feza na zahabu na nguo, akamupa Rebeka. Vilevile aliwapa wandugu na mama ya Rebeka mapambo ya bei kubwa. Mutumishi wa Abrahamu na watu aliokuja nao wakakula, wakakunywa na kulala kule. Walipoamuka asubui, mutumishi yule akasema: “Ninaomba kurudi kwa bwana wangu.” Lakini wandugu na mama ya Rebeka wakasema: “Umwache binti akae nasi muda mufupi, kama siku kumi hivi; kisha anaweza kwenda.” Lakini yeye akasema: “Tafazali, musinicheleweshe, kwa sababu Yawe amekwisha kufanikisha katika safari yangu. Ninaomba muniruhusu kurudi kwa bwana wangu.” Nao wakasema: “Basi, tumwite binti mwenyewe, tumwulize.” Wakamwita Rebeka na kumwuliza: “Utakwenda na mutu huyu?” Naye akajibu: “Nitakwenda.” Basi, wakamwacha Rebeka aende na mutumishi wa Abrahamu na watu wake. Mulezi wa Rebeka vilevile alikwenda naye. Basi, wakamubariki Rebeka wakisema: “Ewe dada yetu! Ukuwe mama wa maelfu kwa maelfu; wazao wako warizi miji ya waadui zao.” Kisha, Rebeka na wajakazi wake wakapanda juu ya ngamia na kumufuata yule mutumishi wa Abrahamu, nao wote wakaondoka. Wakati ule, Isaka alikuwa ameondoka Beri-Lahai-Roi, akakaa pande za Negebu. Siku moja magaribi, Isaka akakwenda kwenye mashamba kwa kufikiri. Basi, akainua macho akaona ngamia wanakuja. Naye Rebeka alipoinua macho na kumwona Isaka, akashuka chini na kumwuliza mutumishi wa Abrahamu: “Ni nani yule mutu anayetembea kule katika shamba, anakuja kutupokea?” Yule mutumishi akasema: “Ni bwana wangu.” Basi, Rebeka akatwaa kitambaa chake, akajifunika uso. Yule mutumishi akamwelezea Isaka yote aliyokuwa ameyafanya. Basi, Isaka akamutwaa Rebeka ndani ya hema iliyokuwa ya mama yake Sara, naye akakuwa muke wake. Isaka akamupenda Rebeka na kupata kufarijika nyuma ya kifo cha mama yake. Abrahamu akaoa muke mwingine, jina lake Ketura. Ketura alimuzalia Abrahamu: Zimurani, Yokisani, Medani, Midiani, Isibaki na Sua. Yokisani alizaa Seba na Dedani. Wazao wa Dedani walikuwa Waashuri, Waletusi na Waleumi. Wana wa Midiani walikuwa Efa, Eferi, Hanoki, Abida na Elda. Wote hao walikuwa wazao wa Ketura. Abrahamu akamurizisha Isaka mali yake yote. Lakini akawapa wana wa habara zake zawadi. Na wakati alipokuwa bado muzima, akawapeleka katika inchi ya upande wa mashariki, mbali na mwana wake Isaka. Abrahamu aliishi miaka mia moja makumi saba na mitano. Kisha kuishi maisha marefu na ya fanaka, akakufa na kukutana na wazee wake. Isaka na Isimaeli, wana wa Abrahamu, wakamuzika baba yao katika pango la Makipela, upande wa mashariki wa Mamure kwenye shamba lililokuwa la Efuroni mwana wa Sohari Muhiti. Abrahamu alikuwa amenunua shamba lile kwa Wahiti. Kule ndiko Abrahamu na muke wake Sara walizikwa. Nyuma ya kifo cha Abrahamu, Mungu alimubariki mwana wake Isaka. Naye Isaka akaishi karibu na kisima cha Beri-Lahai-Roi. Hawa ndio wazao wa Isimaeli mwana wa Abrahamu ambaye Hagari Mumisri aliyekuwa mujakazi wa Sara alimuzalia Abrahamu. Haya ni majina yao kufuatana na kuzaliwa kwao: Nebayoti, muzaliwa wa kwanza, Kedari, Adibeli, Mibusamu, Misima, Duma, Masa, Hadadi, Tema, Yeturi, Nafisi na Kedema. Hao ndio wana wa Isimaeli, waliokuwa shina ya makabila kumi na mawili. Makao na vijiji vyao vilijulikana kwa majina yao. Isimaeli alikuwa na umri wa miaka mia moja makumi tatu na saba alipokufa na kukutana na wazee wake. Wazao wa Isimaeli walikaa katika eneo lililokuwa kati ya Havila na Shuri, upande wa mashariki wa Misri, kuelekea Ashuri. Walikaa kwa utengano na wazao wengine wa Abrahamu. Hawa ndio wazao wa Isaka mwana wa Abrahamu. Isaka alipokuwa na umri wa miaka makumi ine akamwoa Rebeka, binti ya Betueli, Musuria wa Padani-Aramu. Rebeka alikuwa dada ya Labani. Rebeka alikuwa tasa, kwa hiyo Isaka akamwomba Yawe. Naye Yawe akakubali ombi lake, Rebeka akapata mimba. Mimba hiyo ilikuwa ya mapacha. Watoto hao waligongana ndani ya tumbo la Rebeka, naye akasema: “Kama hivi ndivyo mambo yanavyokuwa, kwa nini kuishi?” Basi, akakwenda kumwuliza Yawe. Yawe akamwambia: “Mataifa mawili yako ndani ya tumbo lako; makabila mawili yatakayozaliwa nawe, yatatengana. Moja litakuwa lenye nguvu kuliko lingine, mukubwa atamutumikia mudogo.” Siku zake za kuzaa zilipotimia, Rebeka akazaa mapacha. Wa kwanza alikuwa mwekundu, mwenye nywele mwili wote; hivyo wakamwita Esau. Wa pili alizaliwa akiwa amemushika Esau kisigino, hivyo wakamupa jina Yakobo. Isaka alikuwa na umri wa miaka makumi sita wakati Esau na Yakobo walipozaliwa. Watoto hao wakakomaa. Esau alikuwa mwindaji hodari. Alipenda maisha ya pori. Yakobo alikuwa mutu mutulivu. Alipenda maisha ya nyumba. Basi, Isaka akamupenda Esau kwa sababu alipenda kula nyama wa mawindo yake, lakini Rebeka akamupenda Yakobo. Siku moja, Yakobo alipokuwa anapika muchuzi, Esau akarudi kwa nyumba kutoka katika mawindo akiwa na njaa sana. Kwa hiyo Esau akamwambia Yakobo: “Ninasikia njaa. Tafazali, unigawanyie muchuzi huo mwekundu nikule.” Ndiyo maana walimupanga jina Edomu, maana yake “mwekundu”. Yakobo akajibu: “Kwanza uniuzishie haki yako ya muzaliwa wa kwanza.” Esau akasema: “Sawa! Niko karibu kufa. Haki yangu ya muzaliwa wa kwanza itanifaa nini?” Yakobo akamwambia: “Uniapie kwanza.” Basi, Esau akamwapia na kumwuzishia Yakobo haki yake ya muzaliwa wa kwanza. Halafu Yakobo akamupa Esau mukate na muchuzi wa manjegere. Esau akakula, akakunywa, kisha akaondoka, akajiendea. Hivi ndivyo Esau alivyoizarau haki yake ya muzaliwa wa kwanza. Kisha kukatokea njaa katika inchi ile, nyuma ya ile ya kwanza iliyokuwa kwa wakati wa Abrahamu. Isaka akakwenda Gerari kwa Abimeleki mufalme wa Wafilistini. Yawe akamutokea Isaka na kumwambia: “Usiende Misri, lakini ukae katika inchi nitakayokuambia. Ukae katika inchi hiyo, nami nitakuwa pamoja nawe na kukubariki. Nitatimiza ahadi niliyomupa baba yako Abrahamu, maana nitakupa wewe na wazao wako inchi hizi zote. Nitawazidisha wazao wako wakuwe kama nyota za mbinguni na kuwapa inchi hizi zote. Kutokana na wazao wako, mataifa yote katika dunia yatabarikiwa, kwa sababu Abrahamu alinitii mimi, akashika maagizo yangu, amri zangu, masharti yangu na sheria zangu.” Basi, Isaka akakaa kule Gerari. Watu wa kule walipomwuliza juu ya muke wake, akajibu: “Huyu ni dada yangu.” Aliogopa kusema kwamba ni muke wake kwa kuogopa kwamba wakaaji wa inchi wangemwua kwa sababu ya Rebeka, maana Rebeka alikuwa muzuri sana. Nyuma ya kukaa kule kwa muda murefu, Abimeleki mufalme wa Wafilistini akachungulia kwenye dirisha akamwona Isaka akimukumbatia muke wake Rebeka. Abimeleki akamwita Isaka na kumwambia: “Hakika huyo ni muke wako! Sababu gani ulisema kwamba ni dada yako?” Isaka akajibu: “Kwa sababu niliogopa kwamba ningeuawa kwa sababu yake.” Abimeleki akamwuliza: “Ni jambo gani hili ulilotutendea? Mumoja wa watu wangu angaliweza kulala na muke wako bila wasiwasi, nawe ungekuwa umeleta kosa juu yetu.” Halafu Abimeleki akawaonya watu wote akisema: “Yeyote atakayemugusa mutu huyu au muke wake, atauawa.” Mwaka ule Isaka akapanda mbegu katika inchi ile, akavuna mara mia zaidi, maana Yawe alimubariki, naye akatajirika. Alizidi kupata mali mpaka akakuwa tajiri sana. Alikuwa na makundi ya kondoo, ngombe na watumwa wengi. Kwa hiyo, Wafilistini wakamwonea wivu. Wakaziba visima vyote vya maji ambavyo watumishi wa baba yake Abrahamu walikuwa wamechimba wakati alipokuwa muzima. Halafu Abimeleki akamwambia Isaka: “Ondoka kwetu, maana wewe umetuzidi nguvu.” Basi, Isaka akaondoka kule, akapiga kambi yake katika bonde la Gerari, akakaa kule. Isaka akachimba vile visima vilivyokuwa vimechimbwa wakati Abrahamu baba yake alipokuwa muzima, visima ambavyo Wafilistini walikuwa wameziba nyuma ya kifo cha Abrahamu. Akavipa majina yaleyale baba yake aliyovipa. Lakini watumishi wa Isaka walipochimba katika lile bonde na kupata kisima cha maji yanayobubujika, wachungaji wa pale Gerari wakagombana na wachungaji wa Isaka wakisema: “Maji haya ni yetu.” Hivyo Isaka akakiita kisima hicho “Ugomvi” kwa sababu waligombana naye. Halafu wakachimba kisima kingine, nacho vilevile wakakigombania; hivyo Isaka akakiita kisima hicho “Fitina”. Kisha Isaka akakwenda pahali pengine na kuchimba kisima kingine. Lakini hicho hawakukigombania. Hivyo Isaka akakiita “Nafasi Pana”, akisema: “Sasa Yawe ametuachia nafasi, nasi tutastawi katika inchi hii.” Kutoka kule, Isaka alikwenda Beri-Seba. Usiku uleule Yawe alimutokea na kumwambia: “Mimi ni Mungu wa baba yako Abrahamu. Usiogope; niko pamoja nawe. Nitakubariki na kuwazidisha wazao wako kwa ajili ya Abrahamu, mutumishi wangu.” Kwa hiyo, Isaka akajenga mazabahu kule na kumwabudu Yawe. Akapiga kambi kule, na watumishi wake wakachimba kisima. Abimeleki alitoka Gerari akiwa pamoja na Ahuzati, mushauri wake, na Fikoli, jemadari wa jeshi lake, akamwendea Isaka. Isaka akawauliza: “Kwa nini mumekuja kwangu ijapokuwa munanichukia na mulinifukuza kwenu?” Wao wakamujibu: “Tumeona wazi kwamba Yawe yuko pamoja nawe. Kwa hiyo, tunafikiri inafaa tufanye kiapo pamoja nawe na kufanya agano, kwamba hautatuzuru, nasi vilevile hatutakuzuru. Tulikutendea tu vizuri, tukakuacha uende kwa amani, bila kukutendea ubaya wowote. Na sasa wewe ni mubarikiwa wa Yawe.” Basi, Isaka akawafanyia karamu, nao wakakula na kunywa. Kesho yake wakaamuka asubui mapema na kufanya kiapo. Kisha Isaka akawasindikiza na kuagana nao kwa amani. Siku ileile watumishi wa Isaka walimufikia na kumupasha habari za kile kisima walichokuwa wamechimba, wakasema: “Tumepata maji!” Basi, Isaka akakiita kisima hicho Siba, ni kusema “Kiapo”. Kwa hiyo jina la muji ule ni Beri-Seba hata leo. Esau alipokuwa na umri wa miaka makumi ine, akaoa wake wawili Wahiti: Yuditi binti ya Beri na Basemati binti ya Eloni. Wanawake hao walifanya maisha ya Isaka na Rebeka kuwa machungu. Na ilikuwa wakati Isaka alipokuwa muzee na macho yake yalikuwa zaifu hata hakuweza kuona tena, akaita Esau mwana wake mukubwa, akamwambia: “Mwana wangu!” Naye akaitika: “Niko hapa!” Isaka akasema: “Angalia, mimi ni muzee, wala siku ya kufa kwangu siijui. Basi, twaa silaha zako, maana yake podo na upinde wako, uende katika pori uniwindie nyama. Halafu unitengenezee chakula kitamu, kile ninachopenda, uniletee nikule, nipate kukubariki mbele ya kufa kwangu.” Kumbe, Rebeka alikuwa anasikiliza wakati ule Isaka alipokuwa akiongea na Esau, mwana wake. Kwa hiyo, Esau alipokwenda katika pori kuwinda, Rebeka akamwambia mwana wake Yakobo: “Nimemusikia baba yako akimwambia kaka yako Esau amwindie nyama na kumutengenezea chakula kitamu, akikule, apate kumubariki mbele ya Yawe mbele ya kufa kwake. Sasa mwana wangu, sikiliza maneno yangu na utii ninayokuagiza. Kwenda kwenye kundi la mbuzi uniletee wana-mbuzi wawili wazuri, nimutengenezee baba yako chakula kitamu, kile anachopenda. Kisha utamupelekea baba yako akule, apate kukubariki mbele ya kufa kwake.” Lakini Yakobo akamwambia mama yake Rebeka: “Kumbuka kaka yangu Esau amejaa nywele juu ya mwili, lakini mimi sina. Labda baba atataka kunipapasa, nami nitaonekana kama mudanganyifu, kwa hiyo nitajiletea laana pahali pa baraka.” Mama yake akamwambia: “Laana yako inipate mimi, mwana wangu; wewe fanya ninavyokuagiza. Kwenda uniletee wale wana-mbuzi.” Basi, Yakobo akakwenda kutwaa wana-mbuzi wawili na kuwaletea kwa mama yake. Naye akatayarisha chakula kitamu sawa vile baba yake Isaka alivyopenda. Kisha Rebeka akatwaa nguo bora za Esau, mwana wake mukubwa, alizokuwa nazo kwa nyumba, akamuvalisha Yakobo, mwana wake mudogo. Akafunika mikono yake na sehemu laini ya shingo yake kwa ngozi za wana-mbuzi. Kisha akamupa kile chakula kitamu na mukate aliokuwa ametayarisha. Basi, Yakobo akaingia ndani kwa baba yake, akamwita: “Baba!” Naye akaitika: “Niko hapa! Ni nani wewe mwana wangu?” Yakobo akamujibu baba yake: “Ni mimi Esau, muzaliwa wako wa kwanza. Nimefanya kama ulivyoniagiza. Tafazali baba, amuka uikae ukule nyama ya mawindo yangu kusudi upate kunibariki.” Lakini Isaka akamwuliza: “Imekuwa namna gani hata umepata mawindo upesi hivyo, mwana wangu?” Yakobo akamujibu: “Yawe, Mungu wako, amenifanikisha.” Halafu Isaka akamwambia Yakobo: “Basi, mwana wangu, karibia nipate kukupapasa kusudi nijue kweli kama wewe ndiwe mwana wangu Esau au hapana.” Yakobo akamukaribia baba yake Isaka, naye akamupapasa na kusema: “Sauti ni sauti ya Yakobo, lakini mikono ni mikono ya Esau.” Hakumutambua kwa sababu mikono yake ilikuwa yenye nywele nyingi kama ya Esau kaka yake; kwa hiyo akamubariki. Akamwuliza tena: “Kweli wewe ndiwe mwana wangu Esau?” Naye akamujibu: “Ndiyo.” Basi, baba yake akasema: “Uniletee hiyo nyama nikule mawindo yako mwana wangu, nikubariki.” Kwa hiyo Yakobo akamupelekea chakula, naye akakula; akamupelekea divai vilevile, akakunywa. Halafu baba yake Isaka, akamwambia: “Sogea karibu, mwana wangu, unibusu.” Basi, Yakobo akamukaribia baba yake na kumubusu, na baba yake aliposikia harufu ya nguo zake, akamubariki akisema: “Hii ni harufu nzuri ya mwana wangu. Ni kama harufu ya shamba Yawe alilobariki! Mungu akumiminie umande wa mbinguni, akupe udongo wenye mboleo, ngano na divai kwa wingi. Jamii za watu zikutumikie, na mataifa yainame mbele yako kwa heshima. Ukuwe mutawala wa wandugu zako, na wana wa mama yako wainame mbele yako kwa heshima. Kila mutu anayekulaani alaaniwe, kila mutu anayekubariki abarikiwe!” Isaka alipokwisha kumubariki Yakobo, naye Yakobo alipokuwa angali tu anatoka mbele ya baba yake Isaka, Esau kaka ya Yakobo, akarudi kutoka katika mawindo. Esau vilevile akatengeneza chakula kitamu, akamupelekea baba yake, akamwambia: “Basi baba, amuka ukule nyama ya mawindo yangu mimi mwana wako, upate kunibariki!” Isaka akauliza: “Wewe ni nani?” Naye akamujibu: “Ni mimi mwana wako Esau, muzaliwa wako wa kwanza.” Hapo Isaka akatetemeka sana, akasema: “Ni nani basi yule aliyewinda na kuniletea nyama ya mawindo, nami nimekwisha kula mbele haujakuja? Tena nimekwisha kumubariki. Hakika, amekwisha kubarikiwa!” Esau aliposikia maneno ya baba yake, akalia kilio kikubwa na cha uchungu. Kisha akamwambia baba yake: “Ee baba yangu, unibariki mimi, tafazali!” Lakini Isaka akasema: “Ndugu yako alikuja kwa udanganyifu, naye ametwaa baraka yako.” Esau akasema: “Ndiyo maana anaitwa Yakobo! Ametwaa nafasi yangu mara mbili. Kwanza alitwaa haki yangu ya muzaliwa wa kwanza, na sasa ametwaa baraka yangu.” Kisha akamwuliza baba yake: “Basi, haukuniwekea baraka yoyote?” Isaka akamujibu: “Nimekwisha kumufanya Yakobo kuwa mutawala wako, na kumupa wandugu zake wote kuwa watumishi wake. Nimemupatia ngano na divai. Nikufanyie nini sasa, wewe mwana wangu?” Esau akamwambia baba yake: “Baba, maana yake una baraka moja tu? Unibariki hata mimi, ee baba!” Halafu Esau akalia kwa sauti kubwa. Kwa hiyo Isaka, baba yake, akamwambia: “Makao yako yatakuwa mbali na udongo wenye mboleo, na mbali na umande wa mbinguni. Utaishi kwa upanga wako, na utamutumikia ndugu yako; lakini utakapoasi utaivunja nira yake toka kwenye shingo yako.” Basi, Esau akamuchukia Yakobo kwa sababu ya baraka aliyokuwa amepewa na baba yake. Esau akawaza: “Siku za kilio cha baba zitakapokwisha, ndipo nitakapomwua ndugu yangu Yakobo.” Lakini Rebeka alipojua nia ya mwana wake mukubwa, akamwita mwana wake mudogo Yakobo, akamwambia: “Angalia, ndugu yako Esau anajifariji akikusudia kukuua. Kwa hiyo, mwana wangu, sikiliza maneno yangu. Ondoka ukimbilie kwa kaka yangu Labani kule Harani. Ukae naye kwa muda, mpaka kasirani ya ndugu yako itakapopoa. Kasirani yake itakapopoa juu yako, naye atakapokuwa amesahau mambo uliyomutendea, nitatuma mutu kwa kukutafuta kule. Kwa nini nikufiwe na ninyi wote wawili siku moja?” Rebeka akamwambia Isaka: “Sina raha kabisa katika maisha kwa sababu ya hawa wanawake Wahiti wa Esau. Ikiwa Yakobo ataoa mumoja wa wanawake hawa Wahiti, maisha yangu yana faida gani?” Hivyo Isaka akamwita Yakobo, akamubariki, akamwagiza akisema: “Usioe mwanamuke yeyote Mukanana. Kwenda Padani-Aramu, kwa nyumba ya babu yako Betueli, uoe mumoja kati ya wabinti za mujomba wako Labani. Mungu Mwenye Nguvu akubariki upate wazao wengi na kuongezeka, kusudi ukuwe jamii kubwa ya watu. Akubariki wewe pamoja na wazao wako kama alivyomubariki Abrahamu, upate kurizi inchi ambamo unakaa kama mugeni, inchi ambayo Mungu alimupa Abrahamu!” Basi, Isaka akamutuma Yakobo, naye akakwenda Padani-Aramu kwa Labani, mwana wa Betueli wa Aramu, kaka ya Rebeka, mama ya Yakobo na Esau. Esau akatambua kwamba Isaka alibariki Yakobo na kumutuma aende kuoa kule Padani-Aramu, na kwamba alipomubariki, alimukataza asioe mwanamuke Mukanana. Akatambua vilevile kwamba Yakobo alimutii mama yake na baba yake, akakwenda Padani-Aramu. Basi, Esau akafahamu kwamba baba yake hapendezwi na wanawake wa Kanana. Hivyo, Esau akakwenda kwa Isimaeli, mwana wa Abrahamu, akaoa Mahalati binti ya Isimaeli, dada ya Nebayoti. Yakobo aliondoka Beri-Seba, akaelekea Harani. Alipofika pahali fulani, akalala pale kwa sababu jua lilikuwa limetua. Akatwaa jiwe moja la pahali pale, akaliweka chini ya kichwa chake, akalala. Akaota ndoto, na katika ndoto hiyo, aliona ngazi iliyosimamishwa juu ya dunia na incha yake inafika mbinguni. Wamalaika wa Mungu walikuwa wakipanda na kushuka katika ngazi hiyo. Yawe alisimama juu ya ngazi hiyo, akamwambia: “Mimi ni Yawe, Mungu wa Abrahamu baba yako, na Mungu wa Isaka. Nitakupa inchi unayoilalia wewe na wazao wako. Wazao wako watakuwa wengi kama mavumbi ya dunia, na urizi wao utaenea kila pahali: upande wa magaribi, mashariki, kaskazini na kusini. Kwa njia yako na ya wazao wako, jamaa zote katika dunia zitabarikiwa. Mimi niko pamoja nawe, nitakulinda popote utakapoenda na kukurudisha katika inchi hii. Sitakuacha mpaka nitakapotimiza ahadi niliyokupa.” Kisha Yakobo akaamuka toka usingizi, akasema: “Hakika, Yawe yuko pahali hapa, nami sikujua!” Yakobo akaogopa na kusema: “Pahali hapa panatisha sana! Bila shaka hapa ni nyumba ya Mungu na mulango wa mbinguni.” Yakobo akaamuka asubui mapema, akatwaa lile jiwe alilokuwa ameliweka chini ya kichwa chake, akalisimika kama nguzo na kulitakasa kwa kulimiminia mafuta. Akaita pahali hapo Beteli, ni kusema “Nyumba ya Mungu”. Jina la mbele la muji ule lilikuwa Luzi. Kisha Yakobo akafanya kiapo akisema: “Ikiwa, ee Mungu, utakuwa pamoja nami na kunilinda katika safari yangu, ukinipa chakula na nguo kusudi nirudi katika nyumba ya baba yangu salama, basi, wewe Yawe utakuwa ndiwe Mungu wangu. Nalo jiwe hili nililosimika hapa kama nguzo, litakuwa nyumba yako Mungu, nami nitakupa sehemu ya kumi ya vitu vyote utakavyonipa.” Yakobo aliendelea na safari yake, akafika katika inchi za watu wa upande wa mashariki. Siku moja akaona kisima katika mbuga, na kando yake makundi matatu ya kondoo wakipumzika. Kondoo walikuwa wanakunyweshwa kutoka kisima hicho kilichokuwa kimefunikwa kwa jiwe kubwa. Kwa kawaida, makundi yote ya kondoo yalipokusanyika, wachungaji walirudisha lile jiwe kwa pamoja toka kwenye kisima na kuwakunywesha kondoo. Halafu walifunika tena kisima kwa jiwe lile. Yakobo akawauliza wachungaji: “Wandugu zangu, mumetoka wapi?” Wakamujibu: “Tumetoka Harani.” Naye akawauliza: “Munamufahamu Labani mwana wa Nahori?” Wakamujibu: “Tunamufahamu.” Akaendelea kuwauliza: “Yuko muzima?” Nao wakamujibu: “Yeye ni muzima; hata binti yake Rakeli, yule kule anakuja na kondoo wake!” Kisha Yakobo akawaambia: “Ninaona ingaliki muchana, na si wakati wa kuwakusanya kondoo pamoja. Basi, mukunyweshe kondoo maji, muende kuwachunga.” Lakini wao wakamwambia: “Hatuwezi kufanya hivyo mpaka makundi yote yakuwe yamekusanyika pamoja, jiwe limeviringishwa juu ya kisima, halafu tutakunywesha kondoo.” Yakobo alipokuwa bado anazungumuza na hao wachungaji, Rakeli akafika na kondoo wa baba yake, maana yeye ndiye aliyekuwa akiwachunga. Yakobo akamwona Rakeli, binti ya mujomba wake Labani. Akaona kondoo ambao vilevile ni wa mujomba wake. Akakwenda na kuliviringisha lile jiwe kwenye mudomo wa kisima. Akakunywesha maji kundi la mujomba wake. Kisha Yakobo akamubusu Rakeli na kulia kwa sauti. Akamujulisha Rakeli kwamba yeye ni wa jamaa ya baba yake, na kwamba ni mwana wa Rebeka. Rakeli akakimbia mbio kwa nyumba akamwarifu baba yake. Labani aliposikia habari za mwipwa wake Yakobo, alikwenda mbio kumupokea, akamukumbatia, akamubusu, akamukaribisha ndani ya nyumba yake. Yakobo akamwelezea Labani mambo yote yaliyotokea. Naye Labani akasema: “Hakika, wewe ni jamaa yangu, damu moja nami!” Yakobo akakaa naye kwa muda wa mwezi mumoja. Siku moja Labani akamwambia Yakobo: “Wewe ni jamaa yangu lakini hiyo haisemi kwamba utanitumikia bure. Uniambie unataka mushahara gani!” Sasa, Labani alikuwa na wabinti wawili: mukubwa anayeitwa Lea na mudogo anayeitwa Rakeli. Lea alikuwa na macho zaifu, lakini Rakeli alikuwa muzuri na wa kupendeza. Yakobo akamupenda Rakeli; kwa hiyo akamwambia Labani: “Nitakutumikia miaka saba kwa ajili ya Rakeli, binti yako mudogo.” Labani akamwambia: “Afazali nimwoeshe Rakeli kwako wewe kuliko kumwoesha kwa mutu mwingine yeyote. Endelea kuishi nami.” Basi, Yakobo akamutumikia Labani miaka saba kwa ajili ya Rakeli, lakini kwake muda ule ulikuwa kama siku chache, kwa vile alivyomupenda Rakeli. Kisha Yakobo akamwambia Labani: “Muda wangu umetimia, kwa hiyo unipe muke wangu.” Basi, Labani akafanya karamu na kuwaalika watu wote wa kule. Lakini magaribi, Labani akatwaa Lea, binti yake mukubwa, na kumupeleka kwa Yakobo. Yakobo akalala naye. (Labani akamutoa Zilpa, mujakazi wake, akuwe mutumishi wa Lea.) Asubui, Yakobo akatambua kwamba ni Lea! Basi, akamwuliza Labani: “Umenitendea jambo gani? Si nilikutumikia kwa ajili ya Rakeli? Mbona basi, umenidanganya?” Labani akamujibu: “Katika inchi yetu hatufanyi hivyo. Si desturi yetu kumwoesha binti mudogo mbele ya mukubwa. Umutimizie Lea siku zake saba za ndoa, nasi tutakupa Rakeli kwa utumishi wa miaka saba mingine.” Yakobo akakubali. Na Yakobo alipomutimizia Lea siku zake saba, Labani akamupa Rakeli, binti yake mudogo akuwe muke wake. (Labani akamutoa Biliha, mujakazi wake, akuwe mujakazi wa Rakeli). Basi, Yakobo akalala na Rakeli vilevile. Lakini Yakobo akamupenda Rakeli kuliko Lea. Akamutumikia Labani miaka mingine saba. Yawe alipoona kwamba Lea anachukiwa, akamujalia watoto; lakini Rakeli alikuwa tasa. Lea akapata mimba, akazaa mutoto mwanaume, akamwita Rubeni, akisema: “Yawe ameona mateso yangu; bila shaka sasa mume wangu atanipenda.” Lea akapata mimba tena, akazaa mutoto mwanaume, akamwita Simeoni, akisema: “Yawe amenipa mutoto mwingine mwanaume kwa sababu amesikia jinsi ninavyochukiwa.” Akapata mimba mara nyingine, akazaa mutoto mwanaume, akamwita Lawi, akisema: “Wakati huu mume wangu atajiunga nami, maana nimemuzalia watoto watatu wanaume.” Lea akapata mimba tena, akazaa mutoto mwanaume, akamwita Yuda, akisema: “Mara hii nitamusifu Yawe.” Kisha Lea akaacha kuzaa. Rakeli alipoona kwamba hajamuzalia Yakobo watoto, alimwonea Lea dada yake wivu, akamwambia Yakobo: “Unipatie watoto, kama sivyo, nitakufa.” Yakobo akamukasirikia Rakeli na kumwambia: “Mimi nimekuwa pahali pa Mungu aliyekuzuia kupata watoto?” Rakeli akamujibu: “Mujakazi wangu Biliha yuko. Lala naye kusudi azae watoto pahali pangu, nami vilevile nipate watoto kutokana naye.” Kwa hiyo Rakeli akamupa Yakobo mujakazi wake, Biliha akuwe muke wake, naye akalala naye. Biliha akapata mimba na kumuzalia Yakobo mutoto mwanaume. Rakeli akasema: “Mungu amenitendea sawa, amesikia kilio changu na kunipa mutoto mwanaume.” Akamwita mutoto yule Dani. Biliha, mujakazi wa Rakeli, akapata mimba tena na kumuzalia Yakobo mutoto wa pili mwanaume. Halafu Rakeli akasema: “Nimepigana mapigano makubwa na dada yangu, nami nimeshinda.” Kwa hiyo akamwita mutoto yule Nafutali. Lea alipoona ameacha kuzaa, alimutwaa Zilpa, mujakazi wake, na kumupa Yakobo kusudi akuwe muke wake. Zilpa akamuzalia Yakobo mutoto mwanaume. Lea akasema: “Bahati njema.” Kwa hiyo akamwita mutoto yule Gadi. Zilpa, mujakazi wa Lea, akamuzalia Yakobo mutoto wa pili mwanaume. Lea akasema: “Bahati njema! Sasa wanawake wataniita heri.” Kwa hiyo akamwita mutoto yule Aseri. Ikakuwa wakati wa mavuno ya ngano, Rubeni alikwenda kwenye shamba na kule akapata matunda ya dudai, akamuletea mama yake Lea. Rakeli akamwambia Lea: “Tafazali, unipe sehemu ya dudai za mwana wako.” Lakini Lea akamwambia kwa ukali: “Unazani ni jambo dogo kuninyanganya mume wangu na sasa unataka kutwaa dudai za mwana wangu?” Rakeli akamujibu: “Ikiwa utanipa dudai za mwana wako, Yakobo atalala kwako leo.” Basi, magaribi Yakobo alipokuwa anarudi toka kwenye shamba, Lea alitoka kwenda kumupokea, akamwambia: “Leo unapaswa kulala nami, maana nimekununua kwa dudai za mwana wangu.” Hivyo Yakobo akalala kwa Lea usiku ule. Mungu akasikiliza ombi la Lea, naye akapata mimba na kumuzalia Yakobo mutoto wa tano mwanaume. Lea akasema: “Mungu amenipa mushahara wangu kwa sababu nilimupa mume wangu mujakazi wangu.” Kwa hiyo akamwita mutoto yule Isakari. Lea akapata mimba tena na kumuzalia Yakobo mutoto wa sita mwanaume. Akasema: “Mungu amenipa zawadi bora. Sasa mume wangu ataniheshimu kwa maana nimemuzalia watoto sita wanaume.” Kwa hiyo akamwita mutoto yule Zabuluni. Kisha akazaa mutoto mwanamuke, akamwita Dina. Kisha Mungu akamukumbuka Rakeli, akakubali ombi lake na kumujalia kupata watoto. Rakeli akapata mimba, akazaa mutoto mwanaume, akasema: “Mungu ameniondolea haya yangu.” Kwa hiyo akamwita mutoto yule Yosefu akisema: “Yawe aniongezee mutoto mwingine mwanaume.” Nyuma Rakeli kuzaa Yosefu, Yakobo akamwambia Labani: “Uniruhusu nirudie kwetu, katika inchi yangu. Unipe wake zangu na watoto wangu ambao nimejipatia kutokana na utumishi wangu kwako, niondoke nao. Unajua kwamba nimekutumikia vema.” Lakini Labani akamwambia: “Basi uniruhusu nami niseme. Nimetambua kwa kuaguza kwamba Yawe amenibariki kwa sababu yako. Sema mushahara wako, nami nitakulipa.” Yakobo akamwambia: “Wewe mwenyewe unajua jinsi nilivyokutumikia, na jinsi nilivyowatunza nyama wako. Mbele sijakuja ulikuwa na mali chache tu lakini tangu nifike, mali yako imeongezeka kwa wingi sana, na Yawe amekubariki kila fasi nilikokwenda. Lakini sasa, nitatunza wakati gani jamaa yangu mwenyewe?” Labani akamwuliza: “Nikupatie nini?” Yakobo akamujibu: “Hautanipatia kitu chochote. Nitaendelea kuwatunza nyama wako ikiwa utanifanyia jambo hili: Uniruhusu nipite kati ya nyama wako wote leo, nitenge katika kundi kila nyama mwenye madoadoa na matakamataka, kila nyama mweusi, kati ya kondoo na mbuzi wanaokuwa na madoadoa na matakamataka. Huo ndio utakaokuwa mushahara wangu. Hivyo, siku zinazokuja, uaminifu wangu utaonekana waziwazi utakapokuja kuangalia mushahara wangu. Mbuzi yeyote asiyekuwa na madoadoa au matakamataka, au kondoo yeyote asiyekuwa mweusi akionekana katika kundi langu, yule atakuwa ameibiwa.” Labani akasema: “Sawa! Ikuwe kama vile ulivyosema.” Lakini siku hiyohiyo Labani akakwenda akatenga beberu wote wenye mistari na madoadoa, mbuzi wote dike waliokuwa na madoadoa na matakamataka, kila nyama aliyekuwa na weupe kwenye mwili wake, na kila kondoo mweusi, akawaweka chini ya ulinzi wa wana wake. Labani akajitenga na Yakobo umbali wa mwendo wa siku tatu, naye Yakobo akabaki akichunga nyama wa Labani waliobaki. Basi, Yakobo akatwaa fito mbichi za miti ya mulubna, lozi na mwaramoni, akazimenya maganda mistari nyeupe ionekane katika fito hizo. Akasimamisha fito zile alizomenya maganda mbele ya nyama katika mabirika ya kukunyweshea maji, pahali ambapo nyama walikuja kukunywa maji. Na kwa sababu nyama walipata mimba walipokuja kunywa maji, wakapata mimba mbele ya zile fito; wakazaa nyama wenye mistari, matakamataka na madoadoa. Yakobo akatenga hao wana-kondoo, kisha akawaelekeza kwenye nyama wenye mistari na weusi katika kundi la Labani. Kwa njia hii, Yakobo akajipatia kundi lake mwenyewe, wala hakulichanganya na lile la Labani. Ikakuwa kila mara ulipofika wakati wa nyama wenye afya kupata mimba, Yakobo aliweka zile fito mbele yao katika mabirika ya kukunyweshea maji, kusudi wapate mimba kwenye fito zile. Lakini hakuweka fito zile mbele ya nyama zaifu walipopata mimba. Hivi, nyama zaifu wakakuwa wa Labani, na wenye afya wakakuwa wa Yakobo. Basi, Yakobo akatajirika sana, akakuwa na makundi makubwa ya nyama, wajakazi na watumwa, ngamia na punda. Basi, Yakobo akasikia kwamba wana wa Labani walinungunika na kusema: “Yakobo amepeleka kila kitu cha baba yetu; ndivyo alivyopata kuwa tajiri.” Yakobo alijua vilevile kwamba Labani hakumujali yeye kama pale mbele. Kisha Yawe akamwambia Yakobo: “Rudia katika inchi ya wazee wako na kwa jamaa yako, nami nitakuwa pamoja nawe.” Basi Yakobo akatuma watu kuita Rakeli na Lea kumukutana katika shamba alimokuwa anachunga nyama wake. Yakobo akawaambia: “Unaona kwamba baba yenu hanijali tena kama vile mbele. Lakini Mungu wa baba yangu amekuwa pamoja nami. Munajua kwamba nimemutumikia baba yenu kwa nguvu zangu zote. Hata hivyo yeye amenidanganya na kubadilisha mushahara wangu mara kumi. Lakini Mungu hakumuruhusu kunizuru. Kila mara baba yenu aliposema: ‘Nyama wenye madoadoa ndio watakaokuwa mushahara wako’, basi kundi lote lilizaa nyama wenye madoadoa. Na kila mara aliposema: ‘Nyama wenye mistari ndio watakaokuwa mushahara wako’, basi, kundi lote lilizaa nyama wenye mistari. Ndivyo Mungu alivyotwaa nyama wa baba yenu, akanipa mimi. “Wakati wa nyama kupata mimba niliota ndoto, na katika ndoto hiyo niliona mabeberu wote waliopanda madike walikuwa wenye mistari, madoadoa na matakamataka. Malaika wa Mungu akaongea nami katika ndoto hiyo, akaniita: ‘Yakobo’, nami nikaitika, ‘Niko hapa!’ Naye akaniambia: ‘Angalia mabeberu wote wanaowapanda madike wana mistari, madoadoa na matakamataka. Jambo hili limekuwa hivyo kwa sababu nimeona jinsi Labani alivyokutendea. Mimi ndimi yule Mungu aliyekutokea kule Beteli, pahali pale ulipotakasa lile jiwe kwa kulimiminia mafuta na ambapo ulifanyia kiapo. Sasa ondoka katika inchi hii urudi katika inchi yako.’ ” Rakeli na Lea wakamujibu Yakobo: “Sisi hatuna tena sehemu au urizi wowote katika nyumba ya baba yetu! Tena yeye anatuona sisi kama wageni, kwa maana ametuuzisha. Naye amekula mali yetu. Mali yote ambayo Mungu ametwaa kutoka kwa baba yetu ni yetu, sisi na watoto wetu. Kwa hiyo, fanya yale Mungu aliyokuagiza!” Basi, Yakobo akajitayarisha kusafiri, akawapandisha watoto wake na wake zake juu ya ngamia. Alitwaa nyama wake wote pamoja na mali yote aliyopata kule Padani-Aramu, akaanza safari ya kurudi katika inchi ya Kanana kwa baba yake Isaka. Wakati ule Labani alikuwa amekwenda kukata manyoya ya nyama wake. Hivyo Rakeli akapata nafasi ya kuiba sanamu za miungu ya baba yake. Yakobo akamudanganya Labani wa Aramu kwa kuondoka bila kumujulisha. Basi, Yakobo akatwaa mali yake yote, akatoroka. Kisha kuvuka muto Furati, akaelekea Gileadi, inchi ya milima. Nyuma ya siku tatu, Labani akajulishwa kwamba Yakobo amemutoroka. Basi, Labani akawatwaa wandugu zake, akamufuata Yakobo kwa muda wa siku saba, akamukuta katika milima, katika inchi ya Gileadi. Lakini usiku, Mungu akamutokea Labani wa Aramu katika ndoto, akamwambia: “Ujichunge! Usimwambie Yakobo neno lolote, jema au baya.” Basi, Labani akamufikia Yakobo. Wakati ule Yakobo alikuwa amepiga kambi yake kwenye milima. Labani naye, pamoja na wandugu zake, akapiga kambi yake kwenye milima ya Gileadi. Halafu Labani akamwambia Yakobo: “Umefanya nini? Mbona umenidanganya, ukatwaa wabinti zangu kama vile wafungwa wa vita? Kwa nini ulitoroka kwa siri, ukanidanganya, wala haukuniarifu kusudi nipate kukuaga kwa shangwe, nyimbo, matari na vinubi? Mbona haukunipa wakati wa kubusu wabinti na wajukuu wangu? Kweli umetenda kipumbafu! Nina uwezo wa kukuzuru; lakini Mungu wa baba yako alinitokea usiku wa kuamukia leo, akaniambia nifanye angalisho, akisema: ‘Ujichunge! Usimwambie Yakobo neno lolote, zuri au baya’. Ninajua ulitoroka kwa sababu ya hamu kubwa ya kurudi katika nyumba ya baba yako. Lakini kwa nini uliiba sanamu za miungu yangu?” Yakobo akamujibu: “Niliogopa kwa sababu nilizani ungeninyanganya wabinti zako. Lakini ukipata mumoja kati yetu na sanamu za miungu yako, atakufa! Mbele ya hawa wandugu zetu, onyesha chochote kinachokuwa chako, ukitwae.” Yakobo hakujua kwamba Rakeli alikuwa ameiba sanamu za miungu ya Labani. Basi, Labani akatafuta sanamu hizo za miungu yake katika hema la Yakobo, la Lea na la wale wajakazi wawili; lakini hakuzipata. Akatoka katika hema la Lea na kuingia katika hema la Rakeli. Rakeli alikuwa ametwaa zile sanamu, akazificha chini ya matandiko ya ngamia na kuketi juu yake. Labani akazitafuta katika hema lote; lakini hakuzipata. Halafu Rakeli akamwambia baba yake: “Tafazali baba, usiuzike, maana siwezi kusimama mbele yako kwa sababu niko katika siku zangu.” Basi, Labani akatafuta sanamu za miungu yake, lakini hakuzipata. Kwa hiyo Yakobo akakasirika, akagombana na Labani akisema: “Kosa langu ni nini hata ukanifuatilia namna hii? Umepata kitu gani kinachokuwa chako hata kupekua mizigo yangu yote? Ukiweke mbele ya wandugu zangu na wandugu zako, kusudi wao waamue kati yetu sisi wawili! Nimekaa nawe kwa muda wa miaka makumi mbili. Muda ule wote kondoo wako, wala mbuzi wako hawajapata kuharibu mimba, wala sikukula kondoo dume wa kundi lako. Mimi sikukuletea nyama wako aliyeuawa na nyama wa pori, lakini nilibeba hasara hiyo mimi mwenyewe. Wewe ulinidai nyama aliyeibwa muchana au usiku! Hivyo, muchana nilivumilia jua kali na usiku baridi ilinipiga. Sikuweza kupata usingizi hata kidogo. Kwa miaka makumi mbili hii yote nimeishi katika nyumba yako. Nilikutumikia miaka kumi na mine kwa ajili ya wabinti zako wawili, na miaka sita nikachunga nyama wako. Lakini wewe, ukabadilisha mushahara wangu mara kumi. Kama Mungu wa babu yangu Abrahamu, Mungu ambaye ni kitisho cha Isaka, asingelikuwa upande wangu, hakika ungeliniacha niondoke mikono mitupu. Lakini Mungu aliona mateso yangu na kazi niliyofanya kwa mikono yangu, akakukaripia usiku wa kuamukia leo.” Halafu Labani akamujibu Yakobo: “Wabinti hawa ni wabinti zangu, watoto hawa ni watoto wangu, nyama hawa ni nyama wangu, na yote unayoona hapa ni yangu. Lakini mimi ninaweza kufanya nini leo juu ya hawa wabinti zangu na watoto wao waliowazaa? Basi, tufanye agano mimi nawe, likuwe ushuhuda kati yako nami.” Basi, Yakobo akatwaa jiwe, akalisimika kama nguzo ya ukumbusho. Tena Yakobo akawaambia wandugu zake: “Mukusanye mawe.” Nao wakakusanya mawe na kufanya lundo. Kisha wakakula chakula karibu na lundo lile la mawe. Ile nguzo akaiita Misipa, ni kusema “Nafasi ya Ulinzi”, maana alisema: “Yawe akuwe mulinzi kati yako na mimi tunapokuwa mbali bila kuonana. Kama ukitesa wabinti zangu, au ukioa wanawake wengine zaidi ya hawa, basi ujue kwamba hakuna anayekuwa mushuhuda kati yetu ila Mungu mwenyewe.” Halafu Labani akamwambia Yakobo: “Angalia lundo hili la mawe na nguzo ambayo nimeisimika kati yako nami. Lundo hili na nguzo hii ni ushuhuda kwamba mimi sitaruka lundo hili kuja kwako kukuzuru, wala wewe hautavuka lundo hili na nguzo hii kuja kwangu kunizuru. Mungu wa Abrahamu na Mungu wa Nahori, ataamua kati yetu.” Basi, Yakobo akaapa kwa Mungu ambaye ni kitisho cha baba yake Isaka. Kisha akatoa sadaka kule kwenye mulima na kuwaalika wandugu zake wakule chakula. Kisha kula, wakabaki kule usiku kucha. Asubui mapema Labani akaamuka, akawabusu wajukuu na wabinti zake, akawabariki. Kisha akaondoka, akarudi kwake. Yakobo akaendelea na safari yake. Basi, wamalaika wa Mungu wakakutana naye. Yakobo alipowaona, akasema: “Hii ni kambi ya jeshi la Mungu!” Kwa hiyo akaita pahali pale “Kambi mbili”. Yakobo alituma wajumbe wamutangulie kwenda kwa ndugu yake Esau, kule Seiri, katika inchi ya Edomu. Akawapa maagizo haya: “Mutamwambia bwana wangu Esau hivi: Mutumishi wako Yakobo anasema hivi: ‘Nimekaa mugeni kwa Labani mpaka sasa. Nina ngombe, punda, makundi ya kondoo, watumwa na wajakazi. Ninakutumia ujumbe huu, bwana wangu, kusudi nipate kukubaliwa mbele yako.’ ” Hao wajumbe walikwenda, kisha wakarudi na kumwambia Yakobo: “Tumefika kwa ndugu yako Esau, naye yuko katika njia kuja kukupokea, akiwa na watu mia ine.” Basi, Yakobo akaogopa sana na kufazaika. Akawagawanya katika makundi mawili watu waliokuwa pamoja naye, kondoo, nyama wengine na ngamia, akifikiri: “Kama Esau akikuja na kuliangamiza kundi moja, basi, kundi litakalobaki litaponyoka.” Kisha Yakobo akamwomba Mungu akisema: “Ee Mungu wa babu yangu Abrahamu, Mungu wa baba yangu Isaka! Ewe Yawe uliyeniambia nirudi katika inchi yangu kwa jamaa yangu, ukaniahidi kunitendea mema, sistahili hata kidogo wema wote na uaminifu wote ulionitendea mimi mutumishi wako. Nilipovuka muto Yordani, sikukuwa na kitu isipokuwa fimbo; lakini sasa nina makundi haya mawili. Ninakuomba uniokoe sasa kutoka kwa ndugu yangu Esau, maana nina hofu kwamba atatushambulia na kutuua wote, mama pamoja na watoto. Wewe uliniahidi kunitendea mema na kuwafanya wazao wangu wakuwe wengi kama muchanga wa bahari ambao hauhesabiki kwa wingi wake.” Basi, Yakobo akalala pale usiku ule. Kisha akatenga sehemu ya mali yake, ikuwe zawadi kwa ndugu yake Esau: mbuzi dike mia mbili na mabeberu makumi mbili, kondoo dike mia mbili, na dume makumi mbili, ngamia makumi tatu wanaonyonyesha pamoja na watoto wao, ngombe dike makumi ine, ngombe dume kumi, punda dike makumi mbili, na dume kumi. Akawapatia watumishi wake, kila mumoja kundi lake, akawaambia: “Mutangulie mukiacha nafasi kati ya kundi na kundi katika mustari wenu.” Akamwagiza yule aliyetangulia: “Ndugu yangu Esau atakapokutana nawe na kukuuliza: ‘Wewe ni mutumishi wa nani? Unakwenda wapi? Na nyama hawa ni wa nani?’ Wewe utamujibu: ‘Hii ni mali ya mutumishi wako Yakobo, nayo ni zawadi yako wewe bwana wangu Esau. Tena Yakobo mwenyewe yuko nyuma anafuata.’ ” Akatoa agizo hilohilo kwa mutumishi wa kundi la pili na la tatu na wengine wote, akisema: “Mutamwambia Esau maneno hayohayo mutakapokutana naye. Zaidi ya yote, mutamwambia: ‘Mutumishi wako Yakobo yuko nyuma, anafuata.’ ” Yakobo alifanya hivyo akifikiri: “Pengine nitamutuliza kwa zawadi hizi ninazomutangulizia na kisha nitaweza kuonana naye macho kwa macho; labda atanipokea.” Basi, akatanguliza zawadi zake, lakini yeye mwenyewe akalala katika kambi usiku ule. Usiku uleule Yakobo akaamuka, akatwaa wake zake wawili, wajakazi wake wawili na watoto wake kumi na mumoja, akapita kivuko cha Yaboki. Kisha kuwavukisha ngambo ya kijito wale waliokuwa nao na mali yake yote, Yakobo akabaki peke yake. Kisha mutu mumoja akakuja, akapigana naye mpaka asubui. Mutu yule alipoona kwamba hawezi kumushinda Yakobo, alimugusa Yakobo kwenye maunganio ya kiuno, naye akateguka alipokuwa anapigana naye. Kisha yule mutu akamwambia Yakobo: “Uniache nijiendee, maana kunapambazuka.” Lakini Yakobo akamwambia: “Sitakuacha hata kidogo, mpaka umenibariki!” Naye akamwuliza: “Jina lako nani?” Yeye akamujibu: “Yakobo.” Yule mutu akamwambia: “Hautaitwa Yakobo tena, lakini Israeli, kwa sababu umeshindana na Mungu na wanadamu, ukashinda.” Halafu Yakobo akamwambia: “Tafazali, ninakuomba uniambie jina lako.” Lakini yeye akamwambia: “Kwa nini kuniuliza jina langu?” Kisha akamubariki Yakobo. Yakobo akaita pahali pale Penueli, akisema: “Nimemwona Mungu uso kwa uso, nami sikukufa.” Jua lilikuwa limekwisha kupanda wakati Yakobo alipoondoka Penueli, akakuwa anachechemea kwa sababu ya kiuno chake. Ndiyo maana mpaka leo Waisraeli hawakuli mushipa wa maunganio ya kiuno, kwa maana yule mutu alimugusa Yakobo kwa maunganio katika mushipa wa kiuno chake. Basi, Yakobo akainua macho, akamwona Esau akikuja pamoja na watu mia ine. Halafu, akawagawanya watoto wake kati ya Lea, Rakeli na wale wajakazi wawili. Akawaweka wajakazi na watoto wao mbele, kisha Lea na watoto wake, na nyuma kabisa wakafuata Rakeli na mwana wake Yosefu. Kisha yeye mwenyewe akawatangulia. Akakwenda akiinama uso mpaka chini kwa heshima mara saba, mpaka alipofika karibu na ndugu yake. Basi, Esau akakwenda mbio kumupokea Yakobo, akamukumbatia, kumubusu kwenye shingo, na wote wawili wakalia. Esau alipoinua macho na kuwaona wale wamama na watoto, akauliza: “Ni wa nani hawa unaokuwa nao?” Yakobo akamujibu: “Hawa ni watoto ambao Mungu, kwa neema yake, amenijalia mimi mutumishi wako.” Kisha wale wajakazi wakakaribia pamoja na watoto wao, wakainama kwa heshima. Vilevile Lea akakuja pamoja na watoto wake, akainama kwa heshima. Kwa mwisho Rakeli na Yosefu wakakuja, wakainama kwa heshima. Halafu Esau akauliza: “Kundi lile nililokutana nalo katika njia lina maana gani?” Yakobo akamujibu: “Nilitumaini kupata kukubaliwa mbele yako, ee bwana wangu.” Lakini Esau akasema: “Nina mali ya kutosha, ndugu yangu. Mali yako ikuwe yako mwenyewe.” Yakobo akamwambia: “Hapana! Kama kweli nimekubaliwa mbele yako, ninakusihi uipokee zawadi yangu. Hakika, kuona uso wako ni kama kuona uso wa Mungu, kwa vile ulivyonipokea kwa wema mukubwa. Basi, ninakuomba ukubali zawadi niliyokuletea, kwa sababu hata mimi vilevile Mungu amenineemesha, nami nina mali nyingi.” Ndivyo Yakobo alivyomushawishi Esau, naye akapokea zawadi yake. Esau akasema: “Basi! Tuendelee na safari yetu. Mimi nitakutangulia.” Lakini Yakobo akamwambia: “Bwana wangu, wewe unajua kwamba watoto hawa ni wachanga, na kwamba nyama hawa wananyonyesha, nami ninapaswa kuwatunza. Kama nyama hawa watapelekwa mbio kwa siku moja, wote watakufa. Basi, ninakuomba utangulie, nami nitafuata polepole kadiri ya mwendo wa nyama na watoto, mpaka nitakapokufikia kule Seiri.” Esau akasema: “Heri nikuachie sehemu ya watu wangu.” Lakini Yakobo akasema: “Kuna sababu gani ya kufanya hivyo? Inanitosha kwamba mimi nimepata kukubaliwa mbele yako, ewe bwana wangu.” Basi, siku hiyo Esau akaanza safari ya kurudi Seiri. Lakini Yakobo akasafiri kwenda Sukoti, na kule akajijengea nyumba na vibanda kwa ajili ya nyama wake. Kwa sababu hiyo, pahali hapo pakaitwa Sukoti, ni kusema “Vibanda”. Kutoka Padani-Aramu, Yakobo akafika salama kwa muji wa Sekemu, katika inchi ya Kanana, akapiga kambi yake karibu na muji ule. Sehemu hiyo ya inchi ambako alipiga kambi aliinunua kutoka kwa wazao wa Hamori, baba ya Sekemu, kwa vikoroti mia moja vya feza. Basi, akajenga mazabahu pahali pale na kuiita “Mungu ni Mungu wa Israeli”. Siku moja Dina, binti ya Yakobo na Lea, akakwenda kuwatembelea wanawake wa inchi hiyo. Basi, Sekemu mwana wa Hamori Muhivi, aliyekuwa mukubwa wa inchi hiyo, alipomwona Dina, akamushika, akalala naye kwa nguvu. Lakini Sekemu akavutiwa sana na yule binti, akamupenda hata akaanza kumubembeleza. Kwa hiyo, Sekemu akazungumuza na Hamori baba yake, akamwambia: “Unitwalie binti huyo kuwa muke wangu.” Yakobo akapata habari kwamba Sekemu amemuchafua binti yake Dina; lakini kwa sababu wana wake walikuwa pamoja na nyama kwenye malisho, akanyamaza mpaka waliporudi. Hamori, baba ya Sekemu, akakwenda kwa Yakobo kusudi azungumuze naye, na wakati uleule wana wa Yakobo walirudi kwa nyumba kutoka kwenye malisho. Waliposikia hayo, vijana wale wakaona uchungu mwingi na kukasirika sana, kwa vile Sekemu alikuwa amewafanyia watu wa Israeli ovu hilo la kulala na binti ya Yakobo; maana jambo hilo halipaswi kutendwa. Lakini Hamori akawaambia: “Mwana wangu Sekemu anamupenda sana binti yenu. Basi, tafazali mumuruhusu amwoe. Muache tuoeane: ninyi mutuoeshee wabinti zenu, nanyi muoe wabinti zetu. Kwa hiyo mutaishi pamoja nasi; mutakuwa huru katika inchi hii. Mutaishi humu, mufanye biashara na kujipatia mali.” Vilevile, Sekemu akawaambia baba na wandugu za Dina: “Ninataka kukubaliwa mbele yenu, nami nitawapa ninyi chochote mutakachosema. Muniombe mali na zawadi, hata ikiwa kikubwa namna gani, nami nitatoa, kufuatana na jinsi mutakavyoniambia. Lakini munipatie tu binti huyu kuwa muke wangu.” Basi, wana wa Yakobo wakamujibu Sekemu na baba yake Hamori kwa udanganyifu, kwa sababu Sekemu alikuwa amekwisha kumuchafua dada yao Dina. Wakawaambia: “Hatuwezi kumwoesha dada yetu kwa mutu asiyetahiriwa. Kufanya hivyo ni haya kwetu. Tutakubaliana nanyi tu kwa sharti hili: kwamba mutakuwa kama sisi kwa kumutahiri kila mwanaume kati yenu. Kwa hiyo tutawaoeshea wabinti zetu na kuwaoa wabinti zenu. Tutaishi pamoja nanyi na kuwa jamaa moja. Lakini musipokubaliana nasi na kutahiriwa, basi, sisi tutamutwaa binti yetu na kujiendea yetu.” Pendekezo lao likapendeza Hamori na mwana wake Sekemu. Kijana yule hakusita hata kidogo kutimiza sharti hilo, kwa vile alivyomupenda binti ya Yakobo, ingawa ni yeye ndiye aliyeheshimika kuliko wote katika nyumba yao. Basi, Hamori na mwana wake Sekemu, wakakwenda kwenye mulango wa muji, pahali pa mikutano, wakaongea na watu wao wakisema: “Watu hawa ni warafiki zetu. Tuwakaribishe waishi katika inchi yetu na kufanya biashara, kwa sababu tuko na inchi ya kututosha sisi na wao vilevile; kisha tutaoa wabinti zao na kuwaoshea binti wetu. Lakini wao watakubali kuishi nasi na tutakuwa jamaa moja kwa sharti hili: kwamba tutamutahiri kila mwanaume kati yetu kama vile wao walivyotahiriwa. Hamuoni kwamba nyama wao wa kufugwa na mali yao yote itakuwa mali yetu? Basi, tukubaliane nao kusudi wakae pamoja nasi.” Wanaume wote waliokusanyika kwenye mulango wa muji ule wakakubaliana na Hamori na mwana wake Sekemu. Kisha, wanaume wote wakatahiriwa. Kisha siku tatu, waliotahiriwa wakiwa wangali na maumivu makali, wana wawili wa Yakobo, Simeoni na Lawi, kaka za Dina, wakatwaa panga zao, wakashambulia muji kwa rafla na kuwaua wanaume wote. Wakawaua kwa upanga Hamori na mwana wake Sekemu, wakamutoa Dina katika nyumba ya Sekemu, wakajiendea. Nyuma ya mauaji hayo, wana wengine wa Yakobo wakaingia katika muji na kunyanganya mali yote katika muji ule, kwa sababu dada yao alikuwa amechafuliwa. Walitwaa kondoo na mbuzi, ngombe, punda na chochote kilichokuwa katika muji au katika shamba. Walitwaa mali yote, watoto na wanawake wote na chochote kilichokuwa ndani ya nyumba zao. Basi, Yakobo akamwambia Simeoni na Lawi: “Ninyi mumeniletea taabu kwa kunifanya nichukiwe na wakaaji wa inchi hii ya Wakanana na Waperizi. Mimi sina watu wengi, na kama wakikusanyika kwa kunishambulia wataniangamiza mimi pamoja na jamaa yangu.” Hao wandugu wawili wakajibu: “Ana haki gani ya kumutendea dada yetu kama kahaba?” Siku moja, Mungu akamwambia Yakobo: “Anza safari, uende kuishi Beteli na kunijengea mazabahu kule, mimi Mungu niliyekutokea wakati ulipomukimbia kaka yako Esau.” Basi, Yakobo akawaambia jamaa yake na wote aliokuwa nao: “Mutupilie mbali sanamu za miungu ya kigeni munazokuwa nazo, mujitakase na kubadilisha nguo zenu. Kisha, tutakwenda Beteli kusudi nimujengee Mungu mazabahu, Mungu ambaye alinisaidia siku ya taabu na kuwa nami popote nilipokwenda.” Basi, wakamupa Yakobo sanamu zote za miungu ya kigeni walizokuwa nazo pamoja na pete walizokuwa wamevaa kwa masikio. Na Yakobo akavizika chini ya muti wa mwalo uliokuwa karibu na Sekemu. Yakobo na wana wake walipokuwa wakisafiri, Mungu akawatia hofu wenyeji wa miji yote ya jirani hata hawakusubutu kuwafuatilia. Basi, Yakobo akafika Luzi, maana yake Beteli, katika inchi ya Kanana, pamoja na watu wote aliokuwa nao. Akajenga mazabahu pahali pale na kupaita “Mungu wa Beteli” maana ni pale ndipo pahali Mungu alipojionyesha kwake wakati alipokuwa akimukimbia kaka yake. Debora, mulezi wa Rebeka, akakufa, akazikwa chini ya muti wa mwalo upande wa kusini wa Beteli. Kwa hiyo Yakobo akauita muji ule “Mwalo wa Maombolezo”. Wakati alipokuwa akirudi kutoka Padani-Aramu, Mungu akamutokea tena Yakobo na kumubariki. Mungu akamwambia: “Jina lako ni Yakobo, lakini hautaitwa hivyo tena, lakini sasa jina lako litakuwa Israeli.” Kwa hiyo Yakobo akaitwa Israeli. Tena Mungu akamwambia: “Mimi ni Mungu Mwenye Nguvu. Ujaliwe wazao wengi na kuongezeka. Taifa na kundi la mataifa watatokea kwako na wafalme watatokea katika uzao wako. Inchi niliyowapa Abrahamu na Isaka nitakupa wewe na wazao wako.” Basi, nyuma ya kuongea na Yakobo, Mungu akamwacha na kupanda juu. Yakobo akasimika nguzo ya jiwe la ukumbusho pahali pale Mungu alipozungumuza naye, akaitakasa kwa kuimiminia sadaka ya kinywaji na mafuta. Basi, Yakobo akapaita pahali pale alipozungumuza na Mungu Beteli. Yakobo na jamaa yake yote wakaendelea na safari yao kutoka Beteli. Walipokuwa umbali fulani mbele ya kufika Efurata, Rakeli akashikwa na uchungu mukali wa kuzaa. Naye alipokuwa katika uchungu ule, muzalishaji akamwambia: “Usiogope, umepata mutoto mwingine mwanaume.” Rakeli akiwa karibu kufa, akamupa yule mutoto jina Beni-oni. Lakini baba yake akamwita mutoto yule Benjamina. Basi, Rakeli akakufa na kuzikwa kando ya njia inayokwenda Efurata, ni kusema Betelehemu. Yakobo akasimika nguzo ya ukumbusho juu ya kaburi ya Rakeli ambayo iko mpaka leo. Israeli, ndiye Yakobo, akaendelea na safari yake na kupiga kambi yake ngambo ya munara wa Ederi. Wakati Israeli alipokuwa anakaa katika inchi ile, mwana wake Rubeni, akalala na Biliha, habara ya baba yake. Naye Israeli akasikia habari hizo. Yakobo alikuwa na wana kumi na wawili. Wana wa Lea walikuwa Rubeni, muzaliwa wa kwanza wa Yakobo, Simeoni, Lawi, Yuda, Isakari na Zabuluni. Wana wa Rakeli walikuwa Yosefu na Benjamina. Wana waliozaliwa na Biliha, mujakazi wa Rakeli, walikuwa Dani na Nafutali. Na wana waliozaliwa na Zilpa, mujakazi wa Lea, walikuwa Gadi na Aseri. Hao ndio wana wa Yakobo, aliozaa alipokuwa kule Padani-Aramu. Yakobo akaondoka akakwenda Mamure kwa baba yake Isaka, kule Kiriati-Arba ni kusema Hebroni, pahali ambapo Abrahamu na Isaka walikaa kama wageni. Isaka alipokuwa na miaka mia moja na makumi nane, akiwa muzee wa miaka mingi, akakufa na kukutana na wazee wake. Watoto wake, Esau na Yakobo wakamuzika. Hawa ndio wazao wa Esau ni kusema Edomu. Esau alioa wake Wakanaa: Ada binti ya Eloni Muhiti, Oholibama binti ya Ana, binti ya Sibeoni Muhivi, na Basemati binti ya Isimaeli, dada ya Nebayoti. Ada alimuzalia Esau Elifazi, naye Basemati akamuzalia Reueli. Oholibama alimuzalia Yeusi, Yalamu na Kora. Hao ndio wana wa Esau ambao wake zake walimuzalia alipokaa katika inchi ya Kanana. Kisha, Esau akawatwaa wake zake, watoto wake wanaume na wanawake, watu wote wa nyumba yake, ngombe wake, nyama wake wengine wote na mali yake yote ambayo alikuwa ameipata katika inchi ya Kanana, akahamia pahali pengine, mbali na ndugu yake Yakobo. Alifanya hivyo kwa sababu mali zao zilikuwa nyingi hata wasiweze kuishi pamoja. Inchi walimokaa kama wageni haikuweza kuwatoshelea kwa sababu ya wingi wa nyama wao. Kwa hiyo, Esau akakwenda kukaa katika inchi ya milima ya Seiri. Jina lingine la Esau ni Edomu. Hawa ndio wazao wa Esau, baba ya Waedomu katika inchi ya milima ya Seiri. Wana wa Esau walikuwa Elifazi aliyezaliwa na Ada muke wake, na Reueli aliyezaliwa na Basemati muke wake mwingine. Wana wa Elifazi walikuwa Temani, Omari, Sefo, Gatamu na Kenazi. Elifazi alikuwa na habara, jina lake Timuna. Huyu alimuzalia mwana, jina lake Amaleki. Basemati, muke wa Esau, alizaa Reueli. Wana wa Reueli walikuwa Nahati, Zera, Sama na Miza. Oholibama, binti ya Ana, binti ya Sibeoni, alimuzalia Esau mume wake wana watatu: Yeusi, Yalamu na Kora. Hawa ndio wakubwa wa makabila yaliyotokana na Esau. Elifazi, aliyekuwa muzaliwa wa kwanza wa Esau alizaa Temani, Omari, Sefo, Kenazi, Kora, Gatamu na Amaleki. Kila mumoja wao akiwa mukubwa wa kabila lake. Hao wote ni wana wa Elifazi katika inchi ya Edomu, waliotokana na Ada, muke wa Esau. Reueli mwana wa Esau, alizaa Nahati, Zera, Sama na Miza. Kila mumoja wao akiwa mukubwa wa kabila lake. Hao wote ni wana wa Reueli katika inchi ya Edomu, waliotokana na Basemati, muke wa Esau. Wana wa Oholibama, muke wa Esau, walikuwa Yeusi, Yalamu na Kora. Kila mumoja wao akiwa mukubwa wa kabila lake. Hao wote ni wana wa Oholibama, binti ya Ana, muke wa Esau. Basi, hao ndio wazao wa Esau, maana yake Edomu. Kila mumoja wao akiwa mukubwa wa kabila lake. Hawa ndio wazao wa Seiri, Muhori, na ndio wenyeji wa inchi hiyo: Lotani, Sobali, Sibeoni, Ana, Disoni, Eseri na Disani; kila mumoja wao akiwa mukubwa wa kabila lake kati ya Wahori wa uzao wa Seiri, katika inchi ya Edomu. Wana wa Lotani walikuwa Hori na Hemani; na dada ya Lotani aliitwa Timuna. Wana wa Sobali walikuwa Alwani, Manahati, Ebali, Sefo na Onamu. Wana wa Sibeoni walikuwa Aya na Ana. Ana ndiye aliyeona chemichemi za maji ya moto katika jangwa, alipokuwa anachunga punda wa baba yake Sibeoni. Watoto wa Ana walikuwa Disoni na binti mumoja jina lake Oholibama. Wana wa Disoni walikuwa Hemudani, Esibani, Itirani na Kerani. Wana wa Eseri walikuwa Bilihani, Zawani, na Akani. Wana wa Disani walikuwa Usi na Arani. Basi, hao ndio wakubwa wa Wahori: Lotani, Sobali, Sibeoni, Ana, Disoni, Eseri na Disani; kila mumoja wao akiwa mukubwa wa kabila lake katika inchi ya Seiri. Hawa ndio wafalme waliotawala katika inchi ya Edomu, mbele mufalme yeyote hajawatawala Waisraeli: Bela mwana wa Beori alitawala inchi ya Edomu akiwa na makao yake makubwa katika muji wa Dinihaba. Bela alipokufa, Yobabu mwana wa Zera kutoka Bosira akatawala pahali pake. Yobabu alipokufa, Husamu wa inchi ya Watemani, akatawala pahali pake. Husamu alipokufa, Hadadi mwana wa Bedadi akatawala pahali pake, makao yake makubwa yakiwa katika muji wa Awiti. Huyu ndiye aliyewapiga na kuwashinda Wamidiani katika inchi ya Moabu. Hadadi alipokufa, Samula kutoka Masireka, akatawala pahali pake. Samula alipokufa, Sauli kutoka Rehoboti, muji unaokuwa karibu na muto Furati, akatawala pahali pake. Sauli alipokufa, Bali-Hanani mwana wa Akibori, akatawala pahali pake. Bali-Hanani mwana wa Akibori alipokufa, Hadari akatawala pahali pake, na jina la muji wake likiwa Pau. Muke wa Akibori alikuwa Mehetabeli, binti ya Matiredi, binti ya Mezahaba. Wakubwa wa makabila yaliyotokana na Esau kadiri ya makabila yao na makao yao walikuwa: Timuna, Alwa, Yeteti, Oholibama, Ela, Pinoni, Kenazi, Temani, Mibusari, Magdieli na Iramu. Hao ndio wakubwa wa makabila yaliyotokana na Edomu, maana yake, Esau, baba ya Edomu. Wametajwa kulingana na makao yao katika sehemu za inchi walizorizi. Yakobo akaendelea kukaa katika inchi ya Kanana, ambamo baba yake aliishi kama mugeni. Hizi ndizo habari za ukoo wa Yakobo. Yosefu, akiwa kijana wa umri wa miaka kumi na saba, alikuwa akichunga kondoo na mbuzi pamoja na wandugu zake, wana wa Biliha na Zilpa, wake za baba yake. Yosefu akakuwa anamujulisha baba yake juu ya tabia mbaya za wandugu zake. Israeli alimupenda Yosefu kuliko watoto wake wote kwa sababu alikuwa amezaliwa wakati wa uzee wake. Alimupa Yosefu kanzu nzuri sana. Lakini wandugu zake walipoona kwamba baba yao alimupenda Yosefu kuliko wao, wakamuchukia hata hawakuzungumuza naye kwa amani. Usiku mumoja, Yosefu akaota ndoto, lakini alipowaelezea wandugu zake, wao wakazidi kumuchukia. Aliwaambia: “Musikilize ndoto niliyoota: Niliota kwamba sisi wote tulikuwa katika shamba tukifunga miganda. Kwa rafla muganda wangu ukainuka na kusimama wima. Miganda yenu ikakusanyika kuuzunguka na kuinamia mbele ya muganda wangu.” Wandugu zake wakamwuliza: “Unataka kutuambia kwamba utatutawala? Au utakuwa na mamlaka juu yetu?” Basi, wakazidi kumuchukia kwa sababu ya ndoto na maneno yake. Kisha Yosefu akaota ndoto ingine, akawaelezea wandugu zake akisema: “Musikilize, nimeota ndoto nyingine. Nimeona jua, mwezi na nyota kumi na moja vinainamia mbele yangu.” Lakini alipomwelezea baba yake na wandugu zake ndoto hiyo, baba yake alimukaripia, akisema: “Ni ndoto gani hiyo uliyoota? Itatupasa mimi, mama yako na wandugu zako kuja kuinama chini kwa heshima mbele yako?” Wandugu zake wakamwonea wivu, lakini baba yake akakuwa anafikiri juu ya jambo hilo. Siku moja, wandugu za Yosefu wakakwenda kuchunga nyama wa baba yao karibu na Sekemu. Basi, Israeli akamwambia Yosefu: “Unajua wandugu zako wanachunga nyama kule Sekemu. Kwa hiyo ninataka kukutuma kwao.” Yosefu akajibu: “Niko tayari.” Baba yake akamwambia: “Kwenda uwaangalie wandugu zako na nyama kama wako salama, kisha uniletee habari.” Basi, Yakobo akamutuma Yosefu kutoka bonde la Hebroni. Yosefu alipokaribia Sekemu, mutu mumoja akamukuta akitangatanga katika mbuga, akamwuliza: “Unatafuta nini?” Yosefu akamujibu: “Ninatafuta wandugu zangu. Tafazali, uniambie pahali wanakochungia nyama.” Yule mutu akamwambia: “Bila shaka wamekwisha ondoka, kwa sababu niliwasikia wakisema kwamba wanakwenda Dotani.” Basi, Yosefu akafuata wandugu zake, akawakuta kule Dotani. Wandugu zake walipomwona akiwa mbali na mbele hajafika karibu, wakafanya mupango wa kumwua. Wakaambiana: “Muangalie! Yule mwota ndoto anakuja. Basi, tumwue na kumutupa ndani ya shimo moja. Kisha tutasema kwamba ameuawa na nyama wa pori. Halafu tutaona hizo ndoto zake zitakuwa namna gani.” Lakini Rubeni aliposikia maneno hayo, akataka kumwokoa toka katika mikono yao. Basi akawaambia wandugu zake: “Tafazali, tusimwue. Musimwange damu. Mumutumbukize katika shimo hili hapa katika mbuga, lakini musimuzuru.” Alisema hivyo kusudi aweze kumwokoa Yosefu kutoka mikono yao na kisha amurudishe kwa baba yake. Yosefu alipowafikia wandugu zake, wao wakamvua kanzu yake. Kisha wakamushika na kumutupa ndani ya shimo. Lakini shimo hilo halikukuwa na maji. Walipoikaa kwa kula wakainua macho na kuona kundi la Waisimaeli wakisafiri kutoka Gileadi kwenda Misri. Ngamia wao walikuwa wakibeba ubani, zeri na manemane. Hapo Yuda akawaambia wandugu zake: “Tutapata faida gani tukimwua ndugu yetu na kuficha damu yake? Afazali tumwuzishe kwa hawa Waisimaeli, lakini tusiguse maisha yake, maana yeye ni ndugu yetu; yeye ni damu moja nasi.” Wandugu zake wakakubaliana naye. Wachuuzi Wamidiani walipofika pahali pale, wale wandugu wakamwondoa Yosefu katika shimo, wakamwuzisha kwa Waisimaeli kwa bei ya vikoroti makumi mbili vya feza; nao wakamupeleka Yosefu Misri. Basi, Rubeni aliporudi kwenye lile shimo, hakumwona Yosefu tena, kwa hiyo akararua nguo zake kwa huzuni, akaendea wandugu zake, akawaambia: “Kijana hayuko, nami niende wapi?” Basi, wakachinja mbuzi, wakaitwaa kanzu ya Yosefu na kuichovya katika damu ya yule mbuzi. Kisha wakamupelekea baba yao ile kanzu, wakamwambia: “Tumeokota kanzu hii. Uangalie kama ni ya mwana wako, au hapana.” Baba yao akatambua hiyo kanzu, akasema: “Ndiyo ni kanzu ya mwana wangu! Bila shaka nyama wa pori amemushambulia na kumukula. Hakika Yosefu ameraruliwa vipandevipande.” Halafu Yakobo akararua nguo zake kwa huzuni, akavaa nguo ya gunia katika kiuno. Akamulilia mwana wake kwa muda wa siku nyingi. Watoto wake wanaume na wanawake wakamufikia kwa kumufariji, lakini akakataa kufarijiwa, akisema: “Uniache. Nitaendelea kuomboleza kwa ajili ya mwana wangu, mpaka nitakaposhuka katika kaburi.” Ndivyo baba yake alivyomulilia. Wakati ule, kule Misri, wale Wamidiani wakamwuzisha Yosefu kwa mutu anayeitwa Potifari, mumoja wa wakubwa wa mufalme wa Misri, ambaye alikuwa mukubwa wa waaskari walinzi. Wakati ule, Yuda akatengana na wandugu zake, akakwenda kukaa na mutu mumoja Mwadulami, jina lake Hira. Akiwa kule, Yuda akamwona binti ya Sua Mukanana, akamwoa. Binti ya Sua akapata mimba akazaa mutoto mwanaume, akamwita Eri. Akapata mimba ingine, akazaa mutoto mwanaume, akamwita Onani. Kisha akapata mutoto mwingine mwanamuke, akamwita Sela. Wakati Sela alipozaliwa, Yuda alikuwa Kezibu. Yuda alimwoea mutoto wake wa kwanza Eri mwanamuke anayeitwa Tamari. Lakini Eri, muzaliwa wa kwanza wa Yuda, alikuwa mwovu mbele ya Yawe, hivyo Yawe akamwua. Basi, Yuda akamwambia Onani: “Umutwae muke wa ndugu yako marehemu, maana vile ndivyo inavyokupasa kufanya, upate kumuzalia ndugu yako watoto.” Lakini Onani alijua kwamba hao watoto hawangekuwa wake. Kwa hiyo, alipolala na muke wa ndugu yake, alimwanga chini mbegu ya uzazi, kusudi asimupatie ndugu yake watoto. Tendo hilo likamwuzi Yawe, akamwua Onani vilevile. Halafu Yuda akamwambia Tamari, muke wa mwana wake: “Rudi kwa nyumba ya baba yako, ubaki mujane mpaka wakati mwana wangu Sela atakapokomaa.” Yuda hakutaka Sela naye akufe kama vile wandugu zake. Basi, Tamari akarudi kwa nyumba ya baba yake. Nyuma ya muda, binti ya Sua, muke wa Yuda, akakufa. Yuda alipomaliza kufanya kilio akaondoka na rafiki yake Hira Mwadulami, wakakwenda Timuna kwa kukata manyoya ya kondoo wake. Tamari aliposikia kwamba baba mukwe wake alikuwa katika njia kwenda Timuna kukata manyoya ya kondoo wake, akavua nguo zake za ujane na kujifunika kitambaa. Kisha akaikaa kwenye mulango wa kuingilia Enaimu, kijiji kilichokuwa katika njia kwenda Timuna. Alifanya hivyo kwa vile aliona kwamba Sela alikwisha kuwa mutu muzima, lakini yeye Tamari hakuoeshwa akuwe muke wake. Basi, Yuda alipokuta Tamari pale, alimuzania kuwa mwanamuke kahaba, maana alikuwa akijifunika uso. Halafu, bila kujua kwamba huyo alikuwa muke wa mwana wake, akamwendea pale kando ya njia, akamwambia: “Ninataka kulala nawe.” Tamari akamwuliza: “Utanipa nini upate kulala nami?” Yuda akamujibu: “Nitakupa mwana-mbuzi kutoka kundi langu.” Tamari akamwambia: “Weka rehani kwa kuhakikisha kwamba utaniletea yule mwana-mbuzi.” Yuda akamwuliza: “Unataka nikupe nini kama rehani?” Naye akamujibu: “Unipe hiyo pete na kamba yake pamoja na hiyo fimbo unayoshika.” Basi, Yuda akamupa vitu hivyo vyote, akalala naye. Tamari akapata mimba yake. Basi, Tamari akarudi kwa nyumba akavua kile kitambaa alichojifunika, akavaa tena nguo zake za ujane. Wakati Yuda alipomutuma yule rafiki yake, Mwadulami, amupelekee yule mwanamuke mwana-mbuzi kusudi arudishiwe rehani aliyomwachia, Hira hakumupata. Hira akauliza wenyeji wa Enaimu: “Yuko wapi yule mwanamuke kahaba aliyekuwa kando ya njia karibu na hapa?” Wakamujibu: “Hapa hapajakuwa mwanamuke kahaba.” Basi, huyo rafiki akarudi kwa Yuda, akamwambia: “Sikumupata! Tena wenyeji wa kule wameniambia kwamba hapajakuwa mwanamuke kahaba yeyote kule.” Yuda akasema: “Acha avichukue vitu hivyo. Kama sivyo atatufanya tuchekelewe. Wewe mwenyewe umeona kwamba nilimupelekea mwana-mbuzi, lakini wewe haukumupata.” Kisha miezi mitatu, Yuda akapata habari hii: “Tamari, muke wa mwana wako amekuwa kahaba, tena amepata mimba kwa kufanya ukahaba.” Basi, Yuda akaamuru: “Mumutoshe inje achomwe kwa moto!” Walipokuwa wakimutoa inje, Tamari akatuma ujumbe kwa baba mukwe wake, akisema: “Mwenye vitu hivi ndiye aliyenipa mimba. Kwa hiyo, ninakuomba umutambue mwenye pete hii na kamba yake, na fimbo hii.” Yuda akavitambua vitu hivyo, akasema: “Tamari ni mwenye haki kuliko mimi. Ni kweli, maana sikumwoesha kwa mwana wangu Sela.” Tokea siku hiyo Yuda hakulala tena na Tamari. Wakati wa kuzaa kwa Tamari ulipofika, ikafahamika kwamba alikuwa na mimba ya mapacha. Basi, alipopata uchungu wa kuzaa, pacha mumoja akatoa mukono inje, naye muzalishaji akaufunga kwa uzi mwekundu, akisema: “Huyu ndiye aliyezaliwa kwanza.” Lakini yule mutoto alipourudisha mukono wake ndani, ndugu yake akazaliwa wa kwanza. Muzalishaji akasema: “Mbona wewe umepita kwa nguvu?” Kwa hiyo akaitwa Peresi. Kisha ndugu yake akazaliwa akiwa na ule uzi mwekundu kwenye mukono, naye akaitwa Zera. Basi, Yosefu aliposhushwa kwenda mpaka Misri, Mumisri mumoja anayeitwa Potifari ambaye alikuwa jemadari wa mufalme wa Misri na mukubwa wa waaskari walinzi, akamununua kutoka kwa Waisimaeli waliomuleta Misri. Yawe alikuwa pamoja na Yosefu, akamufanikisha sana. Yosefu akakuwa anakaa katika nyumba ya bwana wake Mumisri. Yule bwana wake akatambua kwamba Yawe alikuwa pamoja na Yosefu, na kwamba ndiye aliyefanikisha mambo yote Yosefu aliyofanya. Basi, Yosefu akapata kukubaliwa mbele ya Potifari, hata akakuwa mutumishi wake wa pekee. Akamufanya musimamizi wa nyumba yake na mwangalizi wa mali yake yote. Tokea wakati Potifari alipomufanya Yosefu kuwa musimamizi wa nyumba yake na mwangalizi wa mali yake, Yawe akabariki nyumba ya yule Mumisri kwa ajili ya Yosefu. Baraka za Yawe zikakuwa juu ya kila kitu alichokuwa nacho, ndani ya nyumba na katika shamba. Kwa sababu hiyo Potifari alimupa Yosefu mamlaka juu ya mambo yake yote, naye Potifari akaacha kushugulika na chochote isipokuwa tu chakula chake mwenyewe. Yosefu alikuwa kijana muzuri na wa kupendeza. Basi, nyuma ya muda fulani, muke wa Potifari akamutamani Yosefu na kumwambia: “Lala na mimi”. Lakini Yosefu akakataa na kumwambia yule muke wa bwana wake: “Sikiliza! Bwana wangu amenipa mamlaka juu ya kila kitu hapa ndani ya nyumba na hajishugulishi na kitu chochote tena. Hapa ndani ya nyumba yeye hana madaraka kuliko mimi. Yeye hakunikataza kushika chochote isipokuwa wewe tu kwa sababu wewe ni muke wake. Nitaweza namna gani basi kufanya uovu mubaya kama ule na kumukosea Mungu?” Yule mwanamuke akaendelea kumushawishi Yosefu siku kwa siku, lakini Yosefu hakumusikiliza wala kukubali kulala naye. Siku moja, Yosefu akaingia ndani ya nyumba kufanya kazi yake kama kawaida, na watumishi wengine hawakukuwa ndani ya nyumba. Basi, muke wa Potifari akamushika nguo yake na kumwambia: “Lala na mimi!” Lakini Yosefu akamwachia nguo yake katika mikono yake, akakimbilia inje. Kwa hiyo, yule mwanamuke alipoona kwamba Yosefu ameacha nguo yake katika mikono yake na kukimbilia inje, akaita watumishi wa nyumba yake na kuwaambia: “Huyu Mwebrania tuliyeletewa anatuzarau. Alikuja kwangu akitaka kunishika kwa nguvu, lakini nikapiga kelele. Aliposikia ninapiga kelele, akaacha nguo yake, akakimbilia inje!” Basi, yule mwanamuke akaweka nguo ile mpaka wakati mume wake aliporudi ndani ya nyumba. Akamwelezea jambo lile akisema: “Huyu mutumishi Mwebrania uliyemuleta kwetu alinifikia kwa kunizarau. Lakini mara tu nilipopiga kelele, akaacha nguo yake na kukimbilia inje.” Basi, bwana wa Yosefu aliposikia maneno ya muke wake, kwamba ndivyo mutumishi wake alivyomutendea, akawaka hasira. Akamutwaa Yosefu na kumutia katika kifungo, pahali wafungwa wa mufalme walipokuwa. Lakini hata mule katika kifungo, Yawe alikuwa pamoja na Yosefu na kumutendea mema, hata kumufanya apate kukubaliwa mbele ya mukubwa wa kifungo. Hivyo mukubwa wa kifungo akamuweka Yosefu akuwe mukubwa wa wafungwa wote mule katika kifungo. Kila kitu kilichofanyika mule kilifanywa kwa mamlaka yake. Yule mukubwa wa kifungo hakujishugulisha tena na kitu chochote Yosefu alichopewa kwa maana Yawe alikuwa pamoja na Yosefu na kufanikisha kila kitu alichofanya. Wakati fulani nyuma ya mambo hayo, wakubwa wawili waliomutumikia mufalme wa Misri wakamukosea. Wakubwa wale walikuwa mutunza vinywaji mukubwa na mupishi mukubwa wa mukate wa mufalme. Mufalme wa Misri akawakasirikia wale wakubwa wake wawili, akawafungia ndani ya nyumba ya mukubwa wa waaskari walinzi, katika kifungo, pahali Yosefu alipofungwa. Mukubwa wa waaskari walinzi akachagua Yosefu awatumikie. Nao wakakuwa katika kifungo kwa muda fulani. Basi, usiku mumoja, yule mutunza vinywaji mukubwa na yule mupishi mukubwa wa mukate wa mufalme, waliota ndoto mule ndani ya gereza, kila mumoja na ndoto yake tofauti. Yosefu alipokwenda kwao asubui na kuwaona, wote wawili walikuwa wenye wasiwasi. Basi, Yosefu akawauliza wakubwa wale wa mufalme waliokuwa katika kifungo pamoja naye katika nyumba ya bwana wake: “Mbona leo muko na nyuso za huzuni?” Wakamujibu: “Tuna huzuni kwa sababu tumeota ndoto na hakuna anayeweza kututafsiria ndoto zetu.” Yosefu akawaambia: “Kutafsiri ndoto si kazi ya Mungu? Basi, muniambie ndoto zenu.” Mutunza vinywaji mukubwa wa mufalme akamwelezea Yosefu ndoto yake, akisema: “Katika ndoto yangu niliona muzabibu mbele yangu, nao ulikuwa na matawi matatu. Mara tu ulipoanza kuchipuka majani, maua yake yakachanua na vishada vyake vikakuwa zabibu zenye kukomaa. Katika mikono yangu nilikuwa na kikombe cha mufalme, basi, nikatwaa zabibu, nikazikamua katika kikombe kile, nikamupa mufalme.” Yosefu akamwambia yule mutumishi: “Tafsiri ya ndoto yako ni hii: yale matawi matatu ni siku tatu. Nyuma ya siku tatu mufalme atakunyanyua kutoka katika kifungo na kukurudisha tena katika cheo chako. Utaweza tena kumupa mufalme kikombe kwa mukono kama ulivyokuwa unafanya pale mbele. Lakini tafazali usinisahau wakati mambo yatakapokuendea wewe vizuri. Unitendee mema na kusema juu yangu mbele ya mufalme, nipate kutoka humu katika kifungo. Maana mimi nilitoroshwa kutoka inchi ya Waebrania na hapa Misri sijafanya kitu chochote kinachostahili nitiwe katika kifungo.” Yule mupishi mukubwa wa mikate alipoona kwamba maelezo yale ni mazuri, akamwambia Yosefu: “Hata mimi niliota ndoto! Katika ndoto yangu nilikuwa nikibeba juu ya kichwa vitunga vitatu vya mikate. Katika kitunga cha juu, kulikuwa aina mbalimbali za mikate kwa ajili ya mufalme. Lakini, ndege walikuwa wakikula kutoka kitunga kile juu ya kichwa changu!” Yosefu akamwambia: “Tafsiri ya ndoto yako ni hii: vile vitunga tatu ni siku tatu. Nyuma ya siku tatu mufalme atakunyanyua kutoka katika kifungo, atainua kichwa chako kusudi akutundike juu ya muti, nao ndege watakula mwili wako.” Ilipotimia siku ya tatu, ambayo ilikuwa siku ya kufanya sikukuu ya kuzaliwa kwake, mufalme wa Misri akafanyia watumishi wake wote karamu. Akatoa katika kifungo mutunza vinywaji wake mukubwa na mupishi mukubwa wa mikate, akawaweka mbele ya wakubwa wake. Kisha akamurudishia mutunza vinywaji cheo chake, apate kumupatia kikombe. Lakini yule mupishi mukubwa wa mikate akamutundika juu ya muti, kama vile Yosefu alivyokuwa amewaelezea ndoto zao. Hata hivyo, yule mutunza vinywaji mukubwa akamusahau Yosefu, pahali pa kumukumbuka. Ilipofika mwisho wa miaka miwili mizima, mufalme wa Misri akaota ndoto: alijikuta amesimama kando ya muto Nili, akaona ngombe saba wazuri na wanono wakitoka ndani ya muto na kula nyasi. Halafu, nyuma ya wale, ngombe wengine saba waliokonda sana wakatoka katika muto Nili, wakakuja na kusimama karibu na wale ngombe wazuri na wanono, kando ya muto. Wale ngombe waliokonda sana wakakula wale wengine saba wazuri na wanono. Hapo mufalme akaamuka toka usingizi. Alipolala tena, akaota mara ya pili. Aliona masuke saba makubwa na mazuri yanachipuka katika bua moja. Halafu, nyuma ya hayo, masuke mengine saba membamba na yaliyokaushwa na upepo mukali wa jangwa yakatokea. Yale masuke saba membamba yakameza yale masuke saba makubwa yaliyojaa ngano. Basi, mufalme alipoamuka akatambua kwamba ilikuwa ndoto. Kulipokuwa asubui, yeye akiwa na wasiwasi sana, aliwaita wachawi wote wa Misri, na wenye hekima, akawaambia ndoto zake. Lakini hakuna hata mumoja aliyeweza kumutafsiria ndoto zile. Halafu, yule mutunza vinywaji mukubwa akamwambia mufalme: “Leo ninakumbuka makosa yangu! Wakati ule ulipotukasirikia sisi watumishi wako, mimi na mupishi mukubwa wa mikate, ulitufungia ndani ya nyumba ya mukubwa wa waaskari walinzi. Usiku mumoja tuliota ndoto, kila mumoja ndoto yake tofauti. Basi, kijana mumoja Mwebrania, mutumishi wa jemadari wa waaskari walinzi, alikuwa pamoja nasi katika kifungo. Tulipomwelezea ndoto zetu, yeye aliweza kutuelezea kila mumoja wetu kulingana na ndoto yake. Alivyoeleza ndivyo ilivyotokea: mimi nikarudishwa ndani ya kazi yangu na yule mupishi mukubwa wa mikate akatundikwa juu ya muti.” Basi, mufalme akaamuru Yosefu aitwe; naye akaondolewa katika kifungo haraka. Kisha kunyoa na kubadilisha nguo zake, Yosefu akakuja mbele yake. Mufalme akamwambia Yosefu: “Mimi nimeota ndoto, lakini hakuna mutu aliyeweza kunitafsiria. Nimesikia sifa zako kwamba wewe ukiambiwa ndoto unaweza kuieleza.” Yosefu akamujibu: “Sina uwezo ule; lakini Mungu atakupa jibu linalofaa.” Halafu mufalme akamwambia Yosefu: “Niliota kwamba nimesimama kando ya muto Nili, nikaona ngombe saba wazuri na wanono wakitoka katika muto na kula nyasi. Hao wakafuatwa na ngombe wengine saba zaifu, wembamba na wamekonda sana. Mimi sijapata kuona ngombe wa hali hiyo katika inchi ya Misri. Basi, wale ngombe waliokonda sana wakakula wale ngombe saba wanono. Lakini hata nyuma ya kuwakula wale wanono, mutu yeyote asingeweza kutambua kwamba wamewakula wenzao, maana walikuwa tu wamekonda sana kama vile mwanzo. Halafu nikaamuka katika usingizi. Kisha nikaota ndoto ingine: nikaona masuke saba mazuri yaliyojaa ngano yakichipuka katika bua moja. Halafu yakafuatwa na masuke mengine saba matupu, membamba na yaliyokaushwa na upepo mukali wa jangwa. Yale masuke saba membamba yakameza yale masuke saba mazuri. Basi, mimi nikawaambia wachawi ndoto hizo lakini hakuna mutu aliyeweza kunifafanulia.” Halafu Yosefu akamwambia mufalme: “Ndoto zako zote mbili zina maana moja tu. Mungu amekufunulia mambo atakayofanya sasa hivi. Ngombe wale saba wazuri ni miaka saba, na yale masuke saba mazuri vilevile ni miaka saba. Ndoto hiyo tafsiri yake ni moja. Wale ngombe saba waliokonda sana, ambao waliwafuata wale wanono, na yale masuke matupu saba, yaliyokaushwa na upepo mukali wa jangwa, maana yake ni miaka saba ya njaa. Kama vile nilivyokuelezea, ee mufalme, Mungu amekufunulia mambo atakayofanya sasa hivi. Kutakuwa miaka saba ya shibe katika inchi nzima ya Misri. Lakini kisha itafuata miaka saba ya njaa, hata hiyo shibe isahaulike kabisa. Njaa hiyo itaangamiza inchi hii. Shibe hiyo itasahaulika kabisa kwa sababu njaa itakayofuata itakuwa kali sana. Ndoto yako ilirudiliwa mara mbili kwa mifano inayofanana kwa kukuonyesha kwamba Mungu ameamua, naye atatimiza jambo hili sasa hivi. “Kwa hiyo inafaa sasa, ee mufalme, uchague mutu mwenye ujuzi na hekima, umupe kazi ya kuangalia inchi yote ya Misri. Tena, ee mufalme, uchague wasimamizi wamoja hapa katika inchi, uwaagize wakusanye sehemu ya tano ya mavuno yote ya Misri katika kipindi hiki cha miaka saba ya shibe. Uwaagize wasimamizi wale wakusanye chakula chote katika miaka saba inayokuja ya mavuno kwa wingi. Ngano hiyo iwekwe chini ya mamlaka yako, ee mufalme, ikuwe akiba ya chakula kwa miji yote, nao waitunze ngano hiyo. Chakula hicho kitakuwa akiba ya kukinga inchi ya Misri isiangamie kutokana na njaa ya miaka saba itakayofuata.” Shauri Yosefu alilotoa likaonekana kuwa jema mbele ya mufalme wa Misri na watumishi wake wote. Kwa hiyo mufalme akawauliza watumishi wake: “Huyu mutu ana roho wa Mungu! Tunaweza kumupata mutu mwingine kama huyu?” Kisha akamwambia Yosefu: “Kwa sababu Mungu amekufunulia haya yote, hakuna mutu mwingine mwenye akili na hekima kama wewe. Wewe ndiwe utakayeisimamia inchi yangu, na watu wangu wote watakuwa chini ya amri yako. Mimi tu ndiye mukubwa kuliko wewe kwa kuwa ninaikalia kiti cha kifalme. Basi, sasa ninakuchagua kuwa mukubwa wa inchi yote ya Misri!” Halafu, mufalme akavua pete yake ya muhuri kwenye kidole chake na kumuvalisha Yosefu. Akamuvalisha na nguo za kitani safi na mukufu wa zahabu kwa shingo. Mufalme akamupandisha katika gari lake la pili na walinzi wakatangulia mbele ya Yosefu wakilalamika kwa sauti na kusema: “Mupige magoti!” Ndivyo mufalme alivyomupa Yosefu madaraka makubwa juu ya inchi yote ya Misri. Zaidi ya hayo, mufalme akamwambia Yosefu: “Mimi ni mufalme wa Misri! Ninasema hivi: mutu yeyote katika inchi nzima ya Misri asiinue mukono wala muguu wake bila ruhusu yako.” Mufalme akamupa Yosefu jina la Kimisri: Safenati-Panea. Akamupa Asenati, binti ya Potifera, kuhani wa muji wa Oni kuwa muke wake. Basi, Yosefu akaanza kutembelea inchi nzima ya Misri. Yosefu alikuwa na umri wa miaka makumi tatu alipoanza kumutumikia mufalme. Alitoka katika nyumba ya mufalme na kuitembelea inchi yote ya Misri. Katika miaka ile saba ya shibe, mashamba ya Misri yakatoa mazao kwa wingi sana. Yosefu akakusanya chakula chote wakati ule wa miaka saba ya shibe na kukiweka akiba katika miji ya Misri. Katika kila muji akaweka akiba ya chakula kutoka mashamba yanayokuwa karibu na muji ule. Yosefu akaweka akiba ya ngano kwa wingi sana ikakuwa nyingi kama muchanga wa bahari, hata isiweze kupimika. Mbele ya miaka ya njaa kuanza, Yosefu alikuwa amekwisha kupata wana wawili kwa muke wake Asenati, binti ya Potifera kuhani wa muji wa Oni. Yosefu akamwita mwana wake wa kwanza Manase, akisema: “Mungu amenifanya nisahau taabu zangu zote na jamaa ya baba yangu.” Mwana wake wa pili akamwita Efuraimu, akisema: “Mungu amenipa watoto katika inchi ya mateso yangu.” Miaka ile saba ya shibe katika inchi ya Misri ikapita. Ikaanza miaka saba ya njaa kama vile Yosefu alivyokuwa amesema pale mbele. Inchi zingine zote zikakuwa na njaa, lakini inchi yote ya Misri ilikuwa na chakula. Wakati wanainchi wa Misri walipoanza kuona njaa, wakamulilia mufalme awape chakula. Naye akawaambia Wamisri wote: “Mwende kwa Yosefu; mufanye neno lolote atakalowaambia.” Njaa ikazidi kuwa kali na kuenea katika inchi yote. Kwa hiyo Yosefu akafungua gala zote, akawauzishia Wamisri chakula. Zaidi ya hayo, watu toka kila pahali katika dunia walikuja Misri kwa Yosefu kununua ngano, maana njaa ilikuwa kali katika dunia yote. Yakobo alipopata habari kwamba kulikuwa ngano kule Misri, akawaambia wana wake: “Mbona munaikaa mukiangaliana tu? Nimesikia kwamba Misri kuna ngano. Muende kule mununue ngano tusikufe na njaa.” Hivyo wandugu kumi za Yosefu wakaenda kwa kununua ngano. Lakini Yakobo hakumwacha Benjamina, ndugu ya Yosefu, aende pamoja nao maana aliogopa kwamba angeweza kupata hasara. Basi, wana wa Israeli wakafika Misri wakiwa kati ya wanunuzi wengine, maana hata katika inchi ya Kanana kulikuwa njaa. Wakati ule Yosefu alikuwa mukubwa kule Misri. Yeye ndiye aliyekuwa akiwauzishia wanainchi ngano. Basi, kaka zake wakakuja na kuinama mbele ya Yosefu kwa heshima. Yosefu alipoona kaka zake akawatambua, lakini akajifanya sawa vile hawafahamu, akasema nao kwa ukali. Akawauliza: “Mumetoka wapi ninyi?” Wakamujibu: “Tumetoka katika inchi ya Kanana, tumekuja kununua chakula.” Ingawa Yosefu aliwatambua kaka zake, wao hawakumutambua. Akakumbuka ndoto zake za zamani juu ya kaka zake, akawaambia: “Ninyi ni wapelelezi. Mumekuja kupeleleza uzaifu wa inchi yetu.” Wao wakamujibu: “Sivyo, bwana wetu. Sisi watumishi wako tumekuja kununua chakula. Sisi ni ndugu, wana wa baba mumoja. Sisi ni watu waaminifu, wala si wapelelezi.” Lakini Yosefu akawaambia: “Sivyo! Mumekuja hapa kwa kupeleleza uzaifu wa inchi yetu.” Wakamwambia: “Sisi, watumishi wako, tuko wandugu kumi na wawili, wana wa mutu mumoja, mwenyeji wa inchi ya Kanana. Mudogo wetu amebaki na baba kwa nyumba na ndugu yetu mwingine ni marehemu.” Lakini Yosefu akawaambia: “Ni kama vile nilivyosema: ninyi ni wapelelezi tu. Hivi ndivyo mutakavyojaribiwa: Ninaapa kwa jina la mufalme wa Misri, kwamba hamutatoka hapa mpaka mudogo wenu atakapokuja. Mutume mumoja wenu amulete yule ndugu yenu mudogo, wakati wengine wenu wanamungoja katika kifungo. Kwa hiyo ukweli wa maneno yenu utajulikana. Kama sivyo, ninaapa kwa jina la mufalme wa Misri kwamba ninyi ni wapelelezi.” Kisha akawatia wote katika kifungo kwa muda wa siku tatu. Siku ya tatu Yosefu akawaambia: “Kwa sababu ninamwogopa Mungu, mufanye hivi kusudi mupate kuishi: kama kweli ninyi ni watu waaminifu, mumoja wenu abaki katika kifungo na wengine wapeleke ngano kwa jamaa zenu wenye njaa. Kisha mumulete kwangu ndugu yenu mudogo. Hii itahakikisha ukweli wa maneno yenu, nanyi hamutauawa.” Basi, wakakubali kufanya hivyo. Kisha wakasemezana wao kwa wao: “Kweli sisi tulimukosea ndugu yetu. Ingawa tulimwona katika taabu, hatukumujali hata alipotusihi. Ndiyo maana taabu hii yote inatupata.” Rubeni akawaambia: “Si niliwaambia tusimuzuru kijana? Lakini ninyi hamukunisikiliza! Sasa tunaazibiwa kwa ajili ya damu yake.” Wao hawakujua kwamba Yosefu alielewa yote yale waliyosema, maana alipoongea nao ilikuwa kwa njia ya mutafsiri. Yosefu akakwenda pembeni, akaanza kulia. Alipotulia, akarudi kuzungumuza nao. Kisha akamukamata Simeoni na kumufunga mbele ya macho yao. Yosefu akatoa amri wajaze mifuko yao na ngano na kumurudishia kila mumoja feza yake katika mufuko wake, na kuwapa chakula cha njia. Wakafanyiwa mambo hayo yote. Wakabebesha punda wao mizigo yao ya ngano, wakaondoka. Ikakuwa walipofika pahali pa kulala wageni kwa njia, mumoja wao akafungua mufuko wake kusudi apate kumukulisha punda wake, akashangaa kukuta feza yake kwenye kinywa cha mufuko wake. Akawaambia wandugu zake: “Feza yangu imerudishwa. Ndio hii hapa kwenye kinywa cha mufuko wangu!” Waliposikia hayo, wakavunjika moyo. Wakaangalia wakiwa wanatetemeka na kuulizana: “Ni jambo gani hili Mungu alilotutendea?” Walipofika katika inchi ya Kanana kwa baba yao Yakobo, wakamwelezea yote yaliyowapata, wakamwambia: “Mukubwa wa inchi ile alisema nasi kwa ukali, na kutuona kwamba sisi ni wapelelezi katika inchi yake. Lakini sisi tukamwelezea kwamba sisi ni watu waaminifu na wala si wapelelezi. Tukamwelezea kwamba sisi tuko wandugu kumi na wawili wa baba mumoja. Mumoja wetu ni marehemu na yule mudogo yuko kwetu katika inchi ya Kanana pamoja na baba yetu. Halafu mukubwa wa inchi hiyo akatuambia: ‘Hivi ndivyo nitakavyotambua kwamba kweli ninyi ni watu waaminifu. Muniachie kwangu ndugu yenu mumoja, nanyi wengine mupeleke ngano kwa jamaa zenu wenye njaa. Kisha muniletee yule ndugu yenu mudogo, na hapo nitajua kwamba ninyi si wapelelezi lakini ni watu waaminifu. Mukifanya hivyo nitamwacha huru ndugu yenu, nanyi mutaruhusiwa kufanya biashara katika inchi hii.’ ” Walipokuwa wanamimina ngano kutoka mifuko yao, wakashangaa kuona kila mumoja wao amerudishiwa kifuko chake na feza ndani ya mufuko wake. Walipoona hayo, wote pamoja na baba yao, wakashikwa na hofu. Baba yao Yakobo, akawaambia: “Munaniondolea watoto wangu! Yosefu hayuko, Simeoni hayuko, sasa munataka kumutwaa Benjamina. Hayo yote yanaanguka juu yangu!” Hapo Rubeni akamwambia baba yake: “Nisipomurudisha Benjamina, uwaue wana wangu wawili. Muache Benjamina katika mikono yangu, nami nitamulinda na kumurudisha kwako.” Lakini baba yake akamujibu: “Mwana wangu hatakwenda nanyi. Ndugu yake amekwisha kufa, naye peke yake ndiye aliyebaki. Mimi ni muzee mwenye imvi. Ikiwa kijana huyu atapatwa na hasara yoyote katika safari mutakayofanya basi, mutaniua kwa huzuni.” Kisha njaa ikazidi kuwa kali katika inchi ya Kanana. Kisha kumalizika kwa kile chakula walichokuwa wamenunua kutoka Misri, Yakobo akawaambia wana wake: “Mwende tena Misri, mutununulie chakula kidogo.” Lakini Yuda akamwambia baba yake: “Yule mutu alituonya vikali, akisema: ‘Sitawapokea musipokuja na ndugu yenu mudogo.’ Kama utakubali ndugu yetu kwenda pamoja nasi, basi tutakwenda kukununua chakula. Lakini ikiwa hautakubali aende nasi, basi, hatutakwenda kule, maana yule mutu alituambia waziwazi: ‘Hamutaniona musipokuja na ndugu yenu mudogo.’ ” Israeli akasema: “Kwa nini mulinitia katika taabu kwa kumwambia yule mutu kwamba muko na ndugu mwingine?” Wakamujibu: “Yule mutu alituuliza kwa makali sana juu ya mambo yetu na jamaa yetu akisema: ‘Baba yenu angali muzima? Muko na ndugu mwingine?’ Hivyo tukamujibu kulingana na maulizo yake. Tungaliweza namna gani kujua kwamba atatuambia: ‘Mulete ndugu yenu?’ ” Yuda akamwambia baba yake Israeli: “Uniruhusu mimi niende naye kusudi tuondoke mara moja, tuende tununue chakula, tusikufe na njaa pamoja nawe na watoto wetu. Mimi mwenyewe nitakuwa rehani kwake. Wewe utanidai mimi. Nisipomurudisha umwone kwa macho yako mwenyewe, kosa likuwe juu yangu milele. Kama tusingalikawia, tungalikuwa tumekwisha kwenda na kurudi mara mbili.” Hapo Israeli, baba yao, akawaambia: “Basi! Kwa vile ni lazima ikuwe hivyo basi, mufanye hivi: mutwae katika mifuko yenu sehemu ya mazao bora ya inchi yetu, mumupelekee zawadi yule mukubwa. Mumupelekee mafuta kidogo ya mukwaju, asali kidogo, ubani, marasi, kungu na lozi. Mupeleke feza mara mbili ya ile inayohitajika, kwa sababu ni lazima murudishe feza ile iliyowekwa kwenye kinywa cha mifuko yenu; pengine ilirudishwa kwa makosa. Mumupeleke vilevile ndugu yenu muende kwa yule mutu. Mungu Mwenye Nguvu awajalie kupata huruma mbele ya mutu yule, awaachie yule ndugu yenu mwingine na Benjamina warudi pamoja nanyi. Kwa upande wangu, ikinipasa kupotelewa na wana wangu, basi!” Basi, wakatwaa zile zawadi na feza mara mbili ya ile ya mbele, wakakwenda Misri pamoja na ndugu yao Benjamina. Walipofika, wakakwenda na kusimama mbele ya Yosefu. Yosefu alipomwona Benjamina pamoja nao, akamwambia musimamizi wa nyumba yake: “Uwapeleke watu hawa kwenye nyumba, uchinje nyama mumoja na kumutengeneza vizuri, maana watu hawa watakula nami chakula cha muchana.” Musimamizi yule akafanya kama vile alivyoagizwa. Akawapeleka wale wageni kwenye nyumba ya Yosefu. Walipoona wamepelekwa kwenye nyumba ya Yosefu, wakashikwa na hofu, wakasema wao kwa wao: “Tumeletwa huku kwa sababu ya ile feza tuliyorudishiwa katika mifuko yetu tulipokuja safari ya kwanza kusudi apate kisingizio cha kutushambulia kwa rafla na kutunyanganya punda wetu na kutufanya watumwa wake.” Kwa hiyo wakamwendea yule musimamizi wa nyumba ya Yosefu wakaongea naye wakiwa kwa mulango, wakamwambia: “Tafazali, bwana! Sisi tulikuja hapa mara ya kwanza kununua chakula. Tulipofika pahali pa kulala wageni kule katika njia, tukafungua mifuko yetu, tukashangaa kukuta feza ya kila mumoja wetu kwenye kinywa cha mufuko wake bila kuguswa. Sasa tumerudisha feza hiyo. Tumeleta na feza ingine kwa kununua chakula. Hatujui ni nani aliyeweka feza yetu katika mifuko yetu.” Yule musimamizi akawajibu: “Musikuwe na wasiwasi, wala musiogope. Bila shaka Mungu wenu, Mungu wa baba yenu, ndiye aliyewarudishia feza katika mifuko yenu. Mimi nilipokea feza yenu.” Kisha akawaletea Simeoni, ndugu yao. Yule musimamizi alipowakaribisha ndani ya nyumba kwa Yosefu, akawapa maji ya kunawa miguu yao, na punda wao akawakulisha. Nao wakatayarisha zawadi zao za kumupa Yosefu, kwa sababu walisikia kwamba watakula pamoja naye. Yosefu, aliporudi kwake, wakamuletea zile zawadi walizokuwa nazo, wakainama mbele yake kwa heshima. Yosefu akawauliza habari zao na kusema: “Mulinielezea habari za muzee, baba yenu. Yuko salama? Angali muzima?” Wakamujibu: “Mutumishi wako, baba yetu, yuko salama na angali muzima.” Kisha wakainama kwa heshima. Yosefu alipoinua macho yake na kumwona Benjamina, ndugu yake, mutoto wa mama yake, akasema: “Huyu ndiye ndugu yenu mudogo muliyeniambia habari zake? Mungu akubariki, mwana wangu!” Yosefu akatoka pahali pale kwa haraka, kwa sababu ya hamu kubwa juu ya ndugu yake, akatafuta pahali pa kulilia. Akaingia ndani ya chumba chake na kuanza kulia. Kisha kunawa uso wake, akatoka, akijikaza, akaamuru wamuletee chakula. Yosefu alitayarishiwa chakula chake peke yake, na wandugu zake wakatayarishiwa peke yao. Vilevile Wamisri waliokula pamoja naye, wakatayarishiwa peke yao, maana ni chukizo kwa Wamisri kula chakula pamoja na Waebrania. Wandugu za Yosefu waliikaa mbele yake kulingana na umri wao, kuanzia wa kwanza mpaka wa mwisho. Wakakuwa wanaangaliana kwa mushangao. Chakula kilikuwa kikitwaliwa kutoka kwenye meza ya Yosefu na kupelekwa kwao, lakini Benjamina alipewa mara tano zaidi ya kipimo wandugu zake walichopewa. Basi, wakakunywa na kufurahi pamoja naye. Kisha Yosefu akamwagiza musimamizi wa nyumba yake akisema: “Ujaze mifuko ya watu hawa ngano kipimo watakachoweza kubeba. Halafu, weka feza ya kila mumoja wao kwenye kinywa cha mifuko wake. Katika mufuko wa yule mudogo kabisa, uweke kile kikombe changu cha feza, pamoja na feza yake.” Yule musimamizi akafanya kama vile alivyoamuriwa na Yosefu. Kulipopambazuka wakaruhusiwa kuondoka pamoja na punda wao. Walipokuwa wamesafiri mwendo mufupi tu kutoka muji, Yosefu akamwambia musimamizi wa nyumba yake: “Haraka! Ufuate wale watu, na utakapowakuta, uwaulize: ‘Kwa nini mumelipa mema muliyotendewa kwa maovu? Kwa nini mumeiba kikombe cha bwana wangu ambacho yeye anakunywa nacho na kukitumia kwa kuaguza? Mumekosa sana kwa kufanya hivyo!’ ” Yule musimamizi alipowakuta akawaambia maneno hayo. Lakini wao wakamwuliza: “Bwana, una maana gani kutuambia maneno kama hayo? Sisi watumishi wako hatuwezi kufanya jambo kama hilo! Kumbuka, bwana, feza tuliyokuta katika kinywa cha mifuko yetu tuliirudisha kutoka katika inchi ya Kanana. Itawezekana namna gani tena tuibe feza au zahabu kutoka nyumba ya bwana wako? Basi, kama akipatikana mumoja wetu ana kikombe hicho, auawe na sisi wengine wote tutakuwa watumwa wako.” Huyo musimamizi akasema: “Sawa. Ikuwe kama mulivyosema. Yeyote atakayepatikana na kikombe hicho, atakuwa mutumwa wangu, lakini wengine wote hamutakuwa na kosa.” Basi, kila mumoja akashusha mufuko wake chini haraka na kuufungua. Yule musimamizi akapekua mifuko yote, akianza na wakubwa wao na kumalizia na mudogo kabisa. Kikombe kikapatikana katika mufuko wa Benjamina. Kwa hiyo wakararua nguo zao kwa huzuni. Kila mumoja wao akamubebesha punda wake muzigo wake, wakarudi kwa muji. Yuda na wandugu zake wakafika kwa Yosefu naye Yosefu alikuwa bado katika nyumba. Basi, wakainama mbele yake kwa heshima, naye Yosefu akawauliza: “Kwa nini mumefanya hivyo? Hamujui kwamba mutu kama mimi nina uwezo wa kuaguza?” Yuda akamujibu: “Tukuambie nini bwana? Tuseme nini kwa kuonyesha kwamba hatuna kosa? Mungu ameyafichua makosa yetu, sisi watumishi wako. Sasa sisi wote tuko watumwa wako, sisi pamoja na yule aliyepatikana na kikombe chako.” Lakini Yosefu akasema: “Hapana! Mimi siwezi kufanya hivyo! Yule tu aliyepatikana na kikombe changu ndiye atakayekuwa mutumwa wangu. Ninyi wengine wote murudi kwa amani kwa baba yenu.” Halafu Yuda akamukaribia Yosefu na kumwambia: “Bwana, ninakuomba uniruhusu mimi mutumishi wako, nijitetee mbele yako kwa maneno machache. Ninakusihi usinikasirikie, maana wewe ni kama mufalme wa Misri mwenyewe. Bwana, wewe ulituuliza kama tuna baba au ndugu, nasi tukakuelezea kwamba tuko na baba, naye ni muzee, na kwamba tuko na ndugu mwingine mudogo aliyezaliwa wakati wa uzee wa baba yetu. Kaka yake na yule kijana amekwisha kufa, na yule mudogo ndiye peke yake aliyebaki wa mama yake; na muzee wetu anamupenda sana kijana yule. Bwana, ulituagiza sisi watumishi wako kumuleta yule mudogo wetu upate kumwona. Tukakuelezea kwamba yule kijana hawezi kuachana na baba yake, kwa sababu akifanya hivyo baba yake atakufa. Lakini wewe bwana ukatuambia kwamba kama hatutakuja na ndugu yetu mudogo, hautatupokea tena. “Tuliporudi kwa mutumishi wako, baba yetu, tulimwarifu ulivyotuagiza, bwana. Naye alipotuambia tukuje tena huku kununua chakula, tukamwambia: ‘Hatuwezi kwenda, isipokuwa tu kama ndugu yetu mudogo atakwenda pamoja nasi. Kama hatakwenda pamoja nasi hatuwezi kupokelewa na yule mutu.’ Basi, baba yetu, mutumishi wako, akatuambia: ‘Munajua kwamba muke wangu Rakeli alinizalia wana wawili: mumoja alitoweka, nami nikasema, bila shaka ameraruliwa vipandevipande na nyama wa pori, maana sijapata kumwona tena. Kama mutamupeleka huyu vilevile kutoka kwangu, akipatwa na hasara, basi mutanishusha katika kaburi nikiwa muzee mwenye huzuni.’ “Kwa hiyo, bwana, siwezi kumurudilia baba yangu, mutumishi wako, bila kijana huyu. Uzima wa baba unategemea uzima wa kijana huyu, na akiona kwamba kijana hayupo pamoja nasi, atakufa! Hivyo sisi watumishi wako tutamwua baba yetu kwa huzuni. Zaidi ya hayo, mimi peke yangu nilijitoa kuwa rehani kwa huyu kijana kwa baba yangu, nikisema: ‘Nisipomurudisha Benjamina kwako, kosa likuwe juu yangu milele.’ Sasa, ee bwana, ninakusihi, mimi mutumishi wako, nibaki, nikuwe mutumwa wako pahali pa kijana huyu. Umwache yeye arudi pamoja na wandugu zake. Nitaweza namna gani kumurudilia baba yangu bila kijana huyu? Siwezi kuvumilia kuona hasara itakayomupata baba yangu.” Halafu Yosefu akashindwa kujizuia mbele ya wote waliokuwa pamoja naye, akawaamuru watoke inje. Hivyo Yosefu alikuwa peke yake alipojitambulisha kwa wandugu zake. Lakini akalia kwa sauti kubwa hata Wamisri wakamusikia. Vilevile watu wa jamaa ya mufalme nao wakamusikia. Yosefu akawaambia wandugu zake: “Mimi ni Yosefu. Baba yangu angali muzima?” Lakini wandugu zake wakapigwa na bumbuazi mbele yake, hata wakashindwa kumujibu. Yosefu akawaambia wandugu zake: “Tafazali, musogee karibu nami.” Walipomukaribia, akawaambia: “Mimi ndiye ndugu yenu Yosefu, muliyemwuzisha Misri. Lakini sasa musifazaike wala kuhuzunika kwa kuniuzisha. Mungu ndiye aliyenileta huku niwatangulie, kusudi niyaokoe maisha ya watu. Huu ni mwaka wa pili tu wa njaa katika inchi, na kungali miaka mitano zaidi ambapo watu hawataweza kulima wala kuvuna mavuno. Mungu alinileta huku niwatangulie ninyi, kwa kuokoa maisha yenu mubaki wazima katika inchi na kuwakomboa kwa ukombozi mukubwa. Kwa hiyo, si ninyi mulionileta huku, lakini ni Mungu. Ndiye aliyenifanya kama baba kwa mufalme wa Misri, musimamizi wa nyumba yake yote na mutawala wa inchi yote ya Misri. “Basi, mufanye haraka! Muende kwa baba na kumwambia: ‘Mwana wako Yosefu anasema: Mungu amenifanya kuwa mukubwa wa inchi yote ya Misri. Basi, usikawie kuja kwangu. Utakaa karibu nami katika eneo la Goseni: wewe, wana wako na wajukuu wako, nyama wako wa kufugwa na mali yako yote. Utakapokuwa Goseni, mimi nitakutunza wewe na jamaa yako pamoja na nyama wako kusudi musikufe na njaa, maana kungali miaka mitano zaidi ya njaa.’ ” Kisha Yosefu akasema: “Ninyi wenyewe mumeona kwa macho yenu na hata ndugu yangu Benjamina ameona kwa macho yake kwamba ni mimi mwenyewe Yosefu ninayezungumuza nanyi. Ni lazima kumwambia baba yangu juu ya utukufu wangu huku Misri na yote muliyoyaona. Basi, mufanye haraka, mumulete baba yangu huku.” Kisha Yosefu akamukumbatia Benjamina, ndugu yake, akalia. Benjamina naye akalia, wakiwa wanakumbatiana. Akiwa angali analia, Yosefu akawakumbatia wandugu zake na kuwabusu. Hapo ndipo wandugu zake walipoweza kuzungumuza naye. Habari zile zilipofika kwa nyumba ya mufalme, kwamba wandugu za Yosefu wamekuja, zikamufurahisha sana na watumishi wake. Kwa hiyo, mufalme akamwambia Yosefu: “Uwaambie wandugu zako wawapakie punda wao mizigo, warudi kwa inchi ya Kanana, wamulete hapa baba yao na jamaa zao wote. Mimi nitawapa sehemu nzuri kabisa ya inchi ya Misri, ambako wataweza kufurahia matunda yote ya inchi hii. Uwaambie vilevile wapeleke kutoka hapa magari ya kukokotwa ya kuwaleta watoto wao wachanga na wake zao. Wala wasikose kumuleta baba yao. Uwaambie wasijali juu ya mali zao, maana sehemu nzuri kuliko zote katika inchi ya Misri itakuwa yao.” Basi, wana wa Israeli wakafanya kama vile walivyoagizwa. Yosefu akawapa magari kulingana na maagizo ya mufalme na chakula cha njia. Aliwapa kila mumoja wao nguo za kubadilisha, lakini akamupa Benjamina vikoroti mia tatu vya feza na nguo tano za kubadilisha. Tena alimupelekea baba yake zawadi hizi kwa ajili ya safari yake: punda kumi waliobeba vitu bora vya Misri, na punda dike kumi waliobeba ngano, mikate na vyakula vingine. Basi, Yosefu akaagana na wandugu zake. Walipokuwa wanaondoka akawaonya akisema: “Musigombane katika njia!” Basi, wakatoka Misri na kurudi kwa baba yao Yakobo, katika inchi ya Kanana. Wakamwambia baba yao: “Yosefu iko muzima! Yeye ndiye mutawala wa inchi yote ya Misri!” Hapo baba yao akapigwa na bumbuazi, maana hakuweza kuyasadiki maneno yao. Lakini, walipomwelezea yote waliagizwa na Yosefu na alipoona magari aliyopelekewa na Yosefu kwa kumubeba, moyo wake ukajaa furaha kupita kiasi. Israeli akasema: “Sasa inatosha! Mwana wangu Yosefu yuko muzima! Nitakwenda nimwone mbele ya kufa kwangu.” Basi, Israeli akaanza safari yake pamoja na mali yake yote. Alipofika Beri-Seba, akatoa sadaka kwa Mungu wa baba yake Isaka. Mungu akaongea na Israeli katika maono usiku, akamwita: “Yakobo! Yakobo!” Yakobo akaitika: “Niko hapa.” Mungu akamwambia: “Mimi ni Mungu, Mungu wa baba yako. Usiogope kwenda Misri. Utakapokuwa kule, nitakufanya kuwa taifa kubwa. Mimi mwenyewe nitakwenda pamoja nawe kule Misri na kukurudisha huku. Utakapokufa, mukono wa Yosefu ndio utakaofumba macho yako.” Basi, Yakobo akaondoka Beri-Seba. Wana wake wakamupeleka yeye, watoto wao wachanga pamoja na wake zao katika magari ambayo mufalme wa Misri alituma kwa kumubeba. Walipeleka vilevile nyama na mali yao yote waliyokuwa wamechuma katika inchi ya Kanana, wakakwenda Misri. Yakobo aliwapeleka wazao wake wote: wana wake, wajukuu wake wanaume na wanawake. Wote akawaleta Misri. Hawa ndio wazao wa Israeli ambao walikwenda Misri pamoja naye: Rubeni, muzaliwa wake wa kwanza, pamoja na wana wa Rubeni: Hanoki, Palu, Hesironi na Karmi. Simeoni na wana wake: Yemueli, Yamini, Ohadi, Yakini, Sohari na Sauli, aliyezaliwa kwa mwanamuke Mukanana. Lawi na wana wake: Gersoni, Kohati na Merari. Yuda na wana wake: Eri, Onani, Sela, Peresi na Zera. (Lakini Eri na Onani walikufa katika inchi ya Kanana). Wana wa Peresi walikuwa Hesironi na Hamuli. Isakari na wana wake: Tola, Puwa, Yasubu na Simuroni. Zebuluni na wana wake: Seredi, Eloni na Yaleli. Hao ndio wana ambao Lea alimuzalia Yakobo kule Padani-Aramu, pamoja na Dina binti yake. Jumla ya wana wake, wabinti zake na wajukuu wake walikuwa watu makumi tatu na watatu. Gadi na wana wake: Sifioni, Hagi, Suni, Esiboni, Eri, Arodi na Areli. Aseri na wana wake: Imuna, Isiwa, Isiwi, Beria na Sera, dada yao. Beria na wana wake: Heberi na Malkieli. Hawa kumi na sita ni wazao wa Yakobo na Zilpa, mujakazi ambaye Labani alimupa binti yake Lea. Rakeli alimuzalia Yakobo wana wawili: Yosefu na Benjamina. Kule Misri, Asenati binti ya Potifera, aliyekuwa kuhani wa muji wa Oni, alimuzalia Yosefu wana wawili: Manase na Efuraimu. Wana wa Benjamina walikuwa Bela, Bekeri, Asibeli, Gera, Namani, Ehi, Rosi, Mupimu, Hupimu na Ardi. Watu hao kumi na wane ni wazao wa Yakobo na muke wake Rakeli. Dani na mwana wake Husimu. Nafutali na wana wake: Yaseli, Guni, Yeseri na Silemu. Hao saba ni wazao wa Yakobo na Biliha, mujakazi ambaye Labani alimupa binti yake Rakeli. Jumla ya wazao wa Yakobo aliokwenda nao Misri, bila kuwahesabu wake za wana wake, ilikuwa watu makumi sita na sita. Kule katika inchi ya Misri Yosefu alikuwa amepata wana wawili. Kwa hiyo watu wote wa jamaa ya Yakobo walioingia Misri walikuwa makumi saba. Yakobo akamutanguliza Yuda kwa Yosefu kumwomba waonane kule Goseni. Nao wakafika katika eneo la Goseni. Yosefu akapanda gari lake la farasi, akakwenda kumupokea baba yake Israeli, kule Goseni. Alipomufikia baba yake, alimukumbatia na kulia kwa kitambo kirefu. Israeli akamwambia Yosefu: “Hata nikikufa sasa si kitu kwa sababu nimeuona uso wako na kujua kwamba wewe uko muzima!” Yosefu akawaambia wandugu zake na jamaa yote ya baba yake: “Ninakwenda kumwarifu mufalme wa Misri kwamba wandugu zangu na jamaa yote ya baba yangu waliokuwa katika inchi ya Kanana wamekuja kwangu. Nitamwelezea kwamba ninyi ni wachungaji maana mumekuwa mukichunga nyama, na kwamba mumefika pamoja na mbuzi, kondoo, ngombe na mali yenu yote. Basi, mufalme akiwaita na kuwauliza: ‘Kazi yenu ni nini?’ Museme: ‘Bwana, sisi watumishi wako, ni wafugaji wa nyama tangu utoto wetu mpaka leo, maana ndivyo babu zetu walivyokuwa.’ Museme hivyo kusudi muruhusiwe kukaa katika eneo la Goseni.” Yosefu alisema hivyo kwa sababu kwa Wamisri wachungaji wote wa kondoo ni chukizo. Basi, Yosefu akakwenda kwa mufalme wa Misri, akamwambia: “Baba yangu na wandugu zangu pamoja na kondoo, ngombe na mali yao yote, wamefika kutoka inchi ya Kanana. Sasa wako katika eneo la Goseni.” Yosefu alikuwa amewatwaa wandugu zake watano, akawajulisha kwa mufalme. Mufalme akawauliza: “Kazi yenu ni nini?” Wakamujibu: “Bwana, sisi watumishi wako ni wachungaji, kama vile babu zetu walivyokuwa.” Kisha wakamwambia mufalme: “Sisi watumishi wako tumekuja kukaa kama wageni katika inchi kwa sababu njaa ni kali kule Kanana na hakuna tena malisho kwa nyama wetu. Hivyo, bwana, tunakuomba, sisi watumishi wako, uturuhusu kukaa katika eneo la Goseni.” Mufalme akamwambia Yosefu: “Baba yako na wandugu zako wamekufikia wewe. Inchi yote ya Misri iko chini yako; uwape baba yako na wandugu zako sehemu bora ya inchi hii. Uwaache wakae katika eneo la Goseni. Na ikiwa unawafahamu watu mashujaa kati yao, uwachague wakuwe waangalizi wa nyama wangu.” Kisha, Yosefu akamuleta baba yake Yakobo kumwamukia mufalme. Naye Yakobo akamupa mufalme baraka zake. Mufalme akamwuliza Yakobo: “Umri wako ni miaka mingapi?” Yakobo akamujibu: “Umri niliojaliwa kama musafiri ni miaka mia moja na makumi tatu. Miaka hiyo imekuwa michache na iliyojaa mateso, tena haijafikia hesabu ya miaka wazee wangu waliyoishi kama wasafiri.” Kisha Yakobo akamubariki mufalme, akaondoka. Basi, Yosefu akawapa baba yake na wandugu zake eneo la Ramesesi lililokuwa bora kabisa katika inchi ya Misri, likuwe makao yao, nao wakalirizi kama vile mufalme alivyoagiza. Yosefu akakuwa anawapatia baba yake, wandugu zake na jamaa yote ya baba yake chakula kulingana na hesabu ya watu waliowategemea. Nyuma chakula kikakosekana kabisa katika inchi yote. Njaa ilikuwa kali sana hata ikawafanya watu wote katika inchi ya Misri na ya Kanana kukonda. Yosefu akakusanya feza yote ya inchi ya Misri na Kanana kutokana na ngano waliyonunua, akapeleka feza hiyo kwa nyumba ya mufalme. Nyuma ya watu wote wa inchi ya Misri na Kanana kutumia feza yao yote, Wamisri wote walimufikia Yosefu na kumwambia: “Utupatie chakula! Kwa nini tukufe mbele ya macho yako? Angalia, sasa feza yetu imekwisha!” Yosefu akawaambia: “Kama feza yenu imekwisha, basi munipe nyama wenu, nami nitawapa ngano.” Halafu wakamuletea Yosefu nyama wao: farasi, ngombe, kondoo, mbuzi na punda, naye akawapa chakula. Mwaka ule Yosefu akakuwa anawapa chakula kwa kubadilishana na nyama wao wote. Mwaka uliofuata wakamufikia tena na kumwambia: “Bwana, ukweli ni kwamba feza yetu yote imekwisha na nyama wetu wamekuwa mali yako. Sasa, bwana, sisi watumishi wako hatuna chochote tunachoweza kukupa isipokuwa miili yetu na mashamba yetu. Kwa nini sisi tukufe mbele ya macho yako na mashamba yetu yaharibike? Utununue sisi pamoja na mashamba yetu, tukuwe watumwa wa mufalme kusudi tupate chakula. Utupatie ngano tusikufe. Utupatie mbegu kwa ajili ya mashamba yetu.” Hivyo Yosefu akainunua inchi yote ya Misri ikuwe mali ya mufalme. Kila Mumisri aliuzisha shamba lake, kwa jinsi njaa ilivyokuwa kali. Inchi yote ikakuwa mali ya mufalme wa Misri, na Yosefu akawafanya watu kuwa watumwa, kutoka pembe moja mpaka pembe ingine ya inchi ya Misri. Udongo ambao Yosefu hakununua ni ule iliokuwa wa makuhani. Hao hawakulazimika kuuzisha udongo wao maana waliishi kwa posho waliyopewa na mufalme. Kisha Yosefu akawaambia watu: “Muangalie, nimekwisha kuwanunua ninyi wote na mashamba yenu kuwa mali ya mufalme. Mutapewa mbegu nanyi mutapanda mashamba yenu. Wakati wa mavuno, sehemu moja ya tano mutamupa mufalme. Sehemu ine zitakazobaki zitakuwa mbegu na chakula kwa ajili yenu na jamaa zenu na watoto wenu.” Wakamujibu: “Bwana, umeyaokoa maisha yetu! Kwa vile umetuonyesha wema wako, sisi tutakuwa watumwa wa mufalme.” Ndivyo Yosefu alivyotangaza sheria moja ambayo iko mpaka leo katika inchi ya Misri. Kila mwanainchi anapaswa kutoa sehemu moja ya tano ya mavuno yake kwa mufalme. Udongo wa makuhani tu ndio haukununuliwa na kufanywa mali ya mufalme. Basi, watu wa Israeli wakakaa katika eneo la Goseni katika inchi ya Misri. Wakiwa kule, wakapata mali nyingi, wakazaa na kuongezeka sana. Yakobo alikaa katika inchi ya Misri kwa muda wa miaka kumi na saba, mpaka alipofikia umri wa miaka mia moja makumi ine na saba. Wakati wa kufa kwake ulipokaribia, Yakobo akamwita mwana wake Yosefu, akamwambia: “Sasa, kama nimepata kukubaliwa mbele yako, weka mukono wako chini ya mapaja yangu, uniahidi kwamba utanitendea kwa wema na uaminifu. Usinizike huku Misri, lakini unilalishe pamoja na babu zangu. Unitwae kutoka Misri na kunizika katika makaburi yao.” Yosefu akamujibu: “Nitafanya kama ulivyosema.” Yakobo akamwambia: “Uniapie!” Yosefu akamwapia. Kisha Israeli akainamia upande wa kichwa cha kitanda chake. Nyuma ya mambo hayo, Yosefu akapewa habari kwamba baba yake ni mugonjwa. Hivyo, akatwaa wana wake wawili, Manase na Efuraimu, akakwenda nao kwa baba yake. Yakobo alipofahamishwa kwamba mwana wake Yosefu amefika kumwona, akajikaza kuamuka, akaikaa juu ya kitanda. Yakobo akamwambia Yosefu: “Mungu Mwenye Nguvu alinitokea nilipokuwa kule Luzu katika inchi ya Kanana, akanibariki. Akaniambia: ‘Nitakufanya ukuwe na wazao na uongezeke. Nitakufanya ukuwe babu ya jamii kubwa za watu. Inchi hii nitawapa wazao wako, wairizi milele.’ ” Yakobo akaendelea kusema: “Wana wako wawili uliowapata hapa Misri mbele sijafika, ni wana wangu. Efuraimu na Manase watakuwa wangu kama vile Rubeni na Simeoni wanavyokuwa. Lakini, watoto utakaopata nyuma watakuwa wako, kwa jina la wandugu zao wataitwa katika urizi wao. Ninaamua hivyo kwa sababu ya mama yako, Rakeli. Nilipokuwa ninarudi kutoka Padani yeye alikufa katika inchi ya Kanana, tukiwa karibu kufika Efurata, akaniachia huzuni. Basi, nikamuzika palepale, kando ya njia inayokwenda Efurata, maana yake Betelehemu.” Israeli alipowaona wana wa Yosefu, akamwuliza: “Ni wa nani hawa?” Yosefu akamujibu baba yake: “Hawa ni wana wangu Mungu alionijalia nikiwa huku.” Israeli akasema: “Tafazali, uwalete karibu nipate kuwabariki.” Macho ya Israeli yalikuwa hayaoni vizuri kwa sababu ya uzee. Basi, Yosefu akasogeza wana wake karibu na baba yake, naye akawabusu na kuwakumbatia. Kisha Israeli akamwambia Yosefu: “Sikutazamia kuuona uso wako tena, lakini, kumbe, Mungu amenijalia hata kuwaona watoto wako!” Hapo Yosefu akawaondoa wana wake kwenye magoti ya baba yake, kisha akainama kwa heshima. Yosefu akawainua wana wake wawili, Efuraimu katika mukono wake wa kuume, akimwelekeza kwenye mukono wa kushoto wa baba yake, na Manase katika mukono wake wa kushoto, akimwelekeza kwenye mukono wa kuume wa baba yake, akawasogeza kwa babu yao. Lakini Israeli akaipishanisha mikono yake: mukono wake wa kuume akauweka juu ya kichwa cha Efuraimu, ingawa alikuwa mudogo na mukono wake wa kushoto akauweka juu ya kichwa cha Manase, aliyekuwa muzaliwa wa kwanza. Kisha Israeli akamubariki Yosefu, akisema: “Mungu ambaye babu zangu Abrahamu na Isaka walimutii katika maisha yao, Mungu ambaye ameniongoza katika maisha yangu mpaka leo, na malaika ambaye aliniokoa katika mabaya yote, awabariki vijana hawa! Jina langu na majina ya babu zangu, Abrahamu na Isaka, yadumishwe katika vijana hawa; nao waongezeke kwa wingi katika dunia.” Yosefu alipoona kwamba baba yake ameuweka mukono wake wa kuume juu ya kichwa cha Efuraimu hakupendezwa. Basi, akaushika mukono wa baba yake, akitaka kuuondoa juu ya kichwa cha Efuraimu auweke juu ya kichwa cha Manase. Akamwambia baba yake: “Sivyo, baba! Huyu hapa ndiye muzaliwa wa kwanza. Tafazali, uweke mukono wako wa kuume juu ya kichwa chake.” Lakini baba yake akakataa, akisema: “Ninajua, mwana wangu, ninajua. Wana wa Manase vilevile watakuwa taifa na wakubwa. Hata hivyo, ndugu yake mudogo atakuwa mukubwa kuliko yeye na wazao wake watakuwa mataifa mengi.” Basi, Israeli akawabariki siku hiyo, akisema: “Waisraeli watatumia majina yenu kwa kubariki, watasema: ‘Mungu akutendee mema kama Efuraimu na Manase!’ ” Ndivyo Israeli alivyomuweka Efuraimu mbele ya Manase. Kisha Israeli akamwambia Yosefu: “Kama vile unavyoona, mimi niko karibu kufa. Hata hivyo, Mungu atakuwa pamoja nanyi, na kuwarudisha katika inchi ya babu zenu. Zaidi ya hayo, nimekupa wewe, wala si wandugu zako, eneo moja kwenye milima, nililowanyanganya Waamori kwa upanga na upinde wangu.” Yakobo akawaita wana wake, akasema: “Mukusanyike pamoja niwaambie mambo yatakayowapata siku zinazokuja. “Mukusanyike musikie, enyi wana wa Yakobo, munisikilize mimi Israeli, baba yenu. “Wewe Rubeni ni muzaliwa wangu wa kwanza, nguvu yangu na tunda la ujana wangu. Wewe unawapita wandugu zako kwa ukubwa na nguvu. Wewe ni kama maji ya mafuriko. Lakini hautakuwa wa kwanza tena, maana ulipanda juu ya kitanda changu mimi baba yako, wewe ulikichafua; hakika wewe ulipanda juu yake! “Simeoni na Lawi ni wandugu: wanatumia silaha zao kutesa kwa ukali, lakini mimi sitashiriki mashauri yao mabaya. Ee roho yangu, usishiriki mikutano yao, maana, katika hasira yao, walimwua mutu, kwa mapenzi yao walikata mushipa wa ngombe. Ninalaani hasira yao kali sana na kasirani yao isiyokuwa na huruma. Nitawatawanya katika inchi ya Yakobo, nitawasambaza katika inchi ya Israeli. “Wewe Yuda, wandugu zako watakusifu. Mukono wako utashika shingo la waadui zako, na wandugu zako watainama mbele yako. Wewe Yuda, mwana wangu, ni kama mwana-simba ambaye amepata mawindo yake akapanda juu, kama simba mukali anajinyoosha na kulala chini. Simba dike, nani anayesubutu kumwamusha? Fimbo ya kifalme haitatoka kwa Yuda, wala bakora ya utawala kwenye miguu yake, mpaka atakapofika yule ambaye ni yake; ambaye mataifa yatamutii. Atafunga punda wake katika muzabibu na mwana-punda wake kwenye muzabibu bora. Atafua nguo zake katika divai, na kanzu zake katika divai nyekundu. Macho yake ni mekundu kwa divai, meno yake ni meupe kwa maziwa. “Zebuluni ataishi pembeni ya bahari, kivuko chake kitakuwa pahali pa kuegesha mashua. Mupaka wa inchi yake ni Sidona. “Isakari ni kama punda mwenye nguvu, anayejilaza kati ya mizigo yake. Aliona kwamba pahali pa kupumzikia ni pazuri, na kwamba inchi ni ya kupendeza, akauinamisha mugongo wake kubeba muzigo, akakuwa mutumwa kwa kufanya kazi za kinguvu. “Dani atakuwa mwamuzi wa watu wake, kama moja ya makabila ya Israeli. Atakuwa kama nyoka katika njia, nyoka mwenye sumu kando ya njia, anayeuma visigino vya farasi, naye mupanda-farasi anaanguka machali. “Ee Yawe, ninangojea uniokoe! “Gadi atashambuliwa na wanyanganyi, lakini yeye atawafuata nyuma na kuwashambulia. “Inchi ya Aseri itatoa mavuno kwa wingi, naye atatoa chakula kinachofaa kwa mufalme. “Nafutali ni kama pongo anayekuwa huru, anayezaa watoto wanaokuwa wazuri. “Yosefu ni kama muti unaozaa, muti unaozaa kando ya chemichemi, matawi yake yanatanda kwenye ukuta. Wapiga mishale walimushambulia vikali, wakamutupia mishale na kumusumbua sana. Lakini upinde wake bado imara, na mikono yake imepewa nguvu, kwa uwezo wa Mwenye Nguvu wa Yakobo, kwa jina la Muchungaji, Mulinzi wa Israeli. Mungu wa baba yako atakusaidia, Mungu Mwenye Nguvu atakubariki, upate baraka za mvua toka juu mbinguni, baraka za maji ya vilindi vinavyokuwa chini, baraka za uzazi wa wamama na nyama. Baraka za baba yako zishinde baraka za milima ya milele, zikuwe bora kuliko vilima vya kale. Baraka hizo zikuwe juu ya kichwa cha Yosefu, juu ya paji lake yeye aliyekuwa ametengwa na wandugu zake. “Benjamina ni imbwa mwitu mukali, asubui anakula mawindo yake, na magaribi anagawanya vitu alivyonyanganya.” Hayo ndiyo makabila kumi na mawili ya Israeli, na hayo ndiyo maneno baba yao aliyowaambia alipowabariki, kila mumoja wao kama alivyostahili. Kisha Israeli akawaagiza wana wake hivi: “Mimi niko karibu kufa na kwenda kukutana na watu wangu. Munizike pamoja na wazee wangu katika pango linalokuwa katika shamba la Efuroni Muhiti, kule Makipela, upande wa mashariki wa Mamure, katika inchi ya Kanana. Abrahamu alinunua pango na shamba hilo kwa Efuroni, Muhiti, likuwe lake la kuzikia. Kule ndiko walikozikwa Abrahamu na muke wake Sara, kule ndiko walikozika Isaka na muke wake Rebeka, na kule ndiko nilikomuzika Lea. Shamba hilo na pango lake lilinunuliwa kwa Wahiti.” Yakobo alipomaliza kuwaagiza wana wake, akarudisha miguu yake juu ya kitanda, akakufa na kukutana na wazee wake. Yosefu akamukumbatia baba yake akilia na kumubusu. Kisha, akawaagiza waganga wake wamupakae baba yake Israeli, dawa kusudi asioze, nao wakafanya hivyo. Kama kawaida, siku makumi ine zilihitajika kwa kazi hiyo. Wamisri nao wakaomboleza kifo cha Yakobo kwa muda wa siku makumi saba. Nyuma ya kilio kumalizika, Yosefu akawaambia watu wa jamaa ya mufalme wa Misri: “Ikiwa nimepata kukubaliwa mbele yenu, tafazali muzungumuze na mufalme kwa ajili yangu kwamba baba yangu aliniapisha, akisema: ‘Mimi niko karibu kufa. Inakupasa kunizika katika kaburi nililojichongea katika inchi ya Kanana.’ Kwa hiyo ninamwomba aniruhusu niende kumuzika baba yangu, kisha nitarudi.” Mufalme akajibu: “Kwenda umuzike baba yako kama vile alivyokuapisha.” Basi, Yosefu akaondoka kwenda kumuzika baba yake akisindikizwa na watumishi wengi wa mufalme wa Misri, wazee wa nyumba ya mufalme, pamoja na wazee wa inchi nzima ya Misri. Vilevile, Yosefu alisindikizwa na jamaa yake yote, wandugu zake na jamaa yote ya baba yake Yakobo. Katika eneo la Goseni kulibaki watoto wao tu pamoja na kondoo, mbuzi na ngombe wao. Vilevile alisindikizwa na wapanda-farasi na magari, lilikuwa kundi kubwa sana. Walipofika katika uwanja wa kupepetea ngano wa Atadi, ngambo ya muto Yordani, waliomboleza kwa huzuni kubwa, naye Yosefu akamufanyia baba yake marehemu kilio cha siku saba. Wakanana wenyeji wa inchi hiyo, walipoona maombolezo yaliyofanyika kwenye uwanja wa kupepetea ngano wa Atadi, wakasema: “Maombolezo haya ya Wamisri, kweli ni makubwa!” Kwa hiyo, pahali pale pakaitwa Abeli-Misri, napo pako ngambo ya muto Yordani. Wana wa Yakobo walimufanyia baba yao kama vile alivyowaagiza: wakamupeleka mpaka inchi ya Kanana, wakamuzika katika pango lililokuwa katika shamba kule Makipela, upande wa mashariki wa Mamure. Pango pamoja na shamba lile Abrahamu alikuwa amelinunua kwa Efuroni Muhiti, kusudi pakuwe pahali pake pa kuzikia. Nyuma ya kumuzika baba yake, Yosefu akarudi Misri pamoja na wandugu zake na watu wote waliokuwa wakimusindikiza kwenda kumuzika baba yake. Nyuma ya kifo cha baba yao, wandugu za Yosefu walisemezana: “Labda Yosefu atatuchukia na kutulipiza mabaya yote tuliyomutendea.” Kwa hiyo wakamupelekea Yosefu ujumbe, wakisema: “Baba yako, mbele hajakufa, aliagiza hivi: ‘Mumwambie Yosefu kwa ajili yangu: Tafazali uwasamehe wandugu zako makosa yao mabaya na maovu yote waliyokutendea.’ Sasa basi, tafazali usamehe uovu tuliokutendea sisi watumishi wa Mungu wa baba yako.” Yosefu alipopata ujumbe huu, akalia. Kisha wandugu zake wakamufikia, wakainama mpaka chini mbele yake, wakasema: “Sisi ni watumishi wako.” Lakini Yosefu akawaambia: “Musiogope, mimi ni pahali pa Mungu? Ninyi mulitaka kunitendea vibaya, lakini Mungu alikusudia mema kusudi watu wengi wapate kuwa wazima kama vile munavyoona leo. Basi, musiogope. Mimi nitawapa chakula pamoja na watoto wenu.” Basi akawafariji na kusema nao vizuri. Yosefu akaendelea kukaa katika inchi ya Misri pamoja na jamaa yote ya baba yake. Aliishi kwa muda wa miaka mia moja na kumi. Yosefu alijaliwa kuwaona watoto na wajukuu wa mwana wake Efuraimu na vilevile kuwapokea kama wana wake watoto wa Makiri mwana wa Manase. Kisha Yosefu akawaambia wandugu zake: “Mimi sasa ninakaribia kufa. Lakini Mungu hakika atawafikia kwa kuwasaidia. Atawatoa katika inchi hii na kuwapeleka katika inchi aliyowaapia Abrahamu, Isaka na Yakobo.” Kisha Yosefu akawaapiza wana wa Israeli, akisema: “Mungu atakapowafikia kwa kuwasaidia, muhakikishe kwamba mutapeleka mifupa yangu kutoka huku.” Basi, Yosefu akakufa kule Misri, akiwa na umri wa miaka mia moja na kumi. Nao wakapakaa mwili wake dawa kusudi usioze, wakauweka katika sanduku kule Misri. Haya ndiyo majina ya wana wa Israeli ambao walikwenda Misri, kila mumoja na jamaa yake: Rubeni, Simeoni, Lawi, Yuda, Isakari, Zebuluni, Benjamina, Dani, Nafutali, Gadi, na Aseri. Wazao wote wa Yakobo walikuwa watu makumi saba. Wakati ule Yosefu alikuwa amekwisha kutangulia kukaa kule Misri. Kisha, Yosefu akakufa, vilevile na wandugu zake na kizazi kile chote. Lakini wazao wa Israeli wakaongezeka sana, wakakuwa wengi na wenye nguvu sana, wakaenea kila pahali katika inchi ya Misri. Basi, kukatokea mufalme mwingine kule Misri ambaye hakumujua Yosefu. Naye akawaambia watu wake: “Muangalie jinsi Waisraeli wanavyokuwa wengi na wenye nguvu kuliko sisi. Ni lazima tutafute werevu wa kuwapunguza na kuzuia wasiongezeke; kama sivyo, vita ikitokea watajiunga na waadui zetu na kutoroka inchi.” Basi, Wamisri wakachagua wakubwa wawasimamie Waisraeli na kuwatesa kwa kazi ngumu. Waisraeli wakafanya kazi ya kumujengea mufalme wa Misri miji ya kuwekea akiba, Pitomu na Ramesesi. Lakini kadiri walivyoteswa ndivyo Waisraeli walivyozidi kuongezeka na kuenea katika inchi. Hivyo Wamisri wakawaogopa sana watu wa Israeli. Basi, Wamisri wakawatumikisha Waisraeli kwa kinguvu. Wakayafanya maisha yao kuwa magumu kwa kazi ngumu ya kutengeneza chokaa na kufyatua matofali, na kazi zote za shamba. Katika kazi zile zote, Waisraeli walitumikishwa kwa kinguvu. Kisha, mufalme wa Misri akawaambia wazalishaji wa Misri, Sifra na Puha, ambao waliwazalisha wanawake Waebrania: “Munapofanya kazi ya kuzalisha wanawake Waebrania, ikiwa mutoto anayezaliwa ni mwanaume, mumwue. Ikiwa ni mwanamuke, mumwache aishi.” Lakini kwa sababu wazalishaji wale walimwogopa Mungu, hawakufanya kama vile walivyoamuriwa na mufalme, lakini waliwaacha watoto wanaume wa Waisraeli waishi. Basi, mufalme akawaita wazalishaji wale, akawauliza: “Kwa nini mumefanya hivyo? Mbona mumewaacha watoto wanaume waishi?” Wao wakamujibu mufalme wa Misri: “Wanawake wa Waebrania si sawa na wanawake Wamisri. Wao ni hodari; mbele muzalishaji hajafika, wao wanakuwa wamekwisha kuzaa.” Basi, Mungu akawajalia mema wazalishaji wale, nao Waisraeli wakazidi kuongezeka na kuwa na nguvu sana. Na kwa sababu wazalishaji wale walimwogopa Mungu, Mungu akawajalia kupata jamaa zao wenyewe. Kisha mufalme wa Misri akawaamuru watu wake wote hivi: “Kila mutoto mwanaume atakayezaliwa kwa Waebrania mumutupe ndani ya muto Nili. Lakini kila mutoto mwanamuke, mumwache aishi.” Kulikuwa mutu mumoja wa ukoo wa Walawi aliyemuoa mwanamuke mumoja ambaye vilevile alikuwa wa ukoo wa Walawi. Basi, mwanamuke yule akapata mimba, akazaa mutoto mwanaume. Alipoona kwamba mutoto yule muchanga alikuwa muzuri, akamuficha kwa muda wa miezi mitatu. Lakini kwa vile hakuweza kumuficha zaidi ya muda ule, akatengeneza namna ya kikapu cha mafunjo, akakipakaa namna ya kabulimbo, akamutia yule mutoto ndani. Kisha akaweka kikapu kando ya muto Nili katika majani. Dada ya yule mutoto akajificha karibu na pahali pale kusudi aone yatakayomupata ndugu yake. Basi, binti ya mufalme wa Misri akashuka kwenye muto kuoga na wajakazi wake wakakuwa wanatembeatembea kandokando ya muto. Binti ya mufalme akaona kile kikapu katika majani, akamutuma mujakazi wake akitwae. Alipokifungua, akamwona yule mutoto muchanga akilia. Basi, akamwonea huruma, akasema: “Huyu ni mumoja wa watoto wa Waebrania.” Palepale dada ya yule mutoto akajitokeza, akamwambia binti ya mufalme: “Niende nikutafutie yaya kati ya wanawake Waebrania akulelee mutoto huyu?” Binti ya mufalme akamwambia: “Kwenda.” Basi, yule binti akaenda, akamwita mama ya yule mutoto. Binti ya mufalme akamwambia yule mama: “Utunze mutoto huyu, umulee kwa ajili yangu, nami nitakulipa mushahara wako.” Basi, yule mama akamutwaa mutoto, akamulea. Mutoto alipokuwa mukubwa, mama yake akamupeleka kwa binti ya mufalme, naye akamutwaa na kumufanya mwana wake. Binti ya mufalme akasema: “Nimemutoa ndani ya maji,” kwa hiyo akamupa mutoto yule jina Musa. Siku moja, Musa alipokuwa mutu muzima, akawaendea Waebrania wenzake kwa kujionea taabu zao. Basi, akamwona Mumisri mumoja akimupiga Mwebrania, mumoja wa wandugu zake. Musa akaangalia huku na huko na alipoona kwamba hakuna mutu karibu, akamwua yule Mumisri na kumuficha ndani ya muchanga. Kesho yake, Musa akatoka tena, akaona Waebrania wawili wakipigana. Basi, akamwuliza yule aliyekosa: “Kwa nini unamupiga mwenzako?” Naye akamujibu: “Nani aliyekuweka wewe kuwa mukubwa na mwamuzi wetu? Unataka kuniua kama vile ulivyomwua yule Mumisri?” Kwa hiyo, Musa akaogopa na kufikiri: “Bila shaka jambo hilo limejulikana!” Naye mufalme wa Misri aliposikia juu ya tukio hilo akakusudia kumwua Musa. Lakini Musa akamukimbia mufalme, akaenda kukaa katika inchi ya Midiani. Siku moja, Musa alikuwa akikaa kando ya kisima cha maji. Basi, wabinti saba wa kuhani mumoja wa kule Midiani wakafika kuchota maji na kuwakunywesha kondoo na mbuzi wa baba yao. Wachungaji wengine wakakuja na kuwafukuza wale wabinti. Lakini Musa akawasaidia wabinti wale na kuwakunywesha nyama wao. Walipomurudilia baba yao Rueli, yeye akawauliza: “Mbona leo mumerudi upesi hivyo?” Nao wakamujibu: “Mumisri mumoja alituokoa toka mikono ya wale wachungaji, naye mwenyewe akachota maji na kuwakunywesha nyama wetu.” Baba yao akawauliza wabinti zake: “Yuko wapi? Mbona mumemwacha kule? Mumwite akuje akule chakula.” Musa akakubali kukaa kwa yule mutu. Basi, yule mutu akamupa Musa binti yake anayeitwa Zipora akuwe muke wake. Zipora akamuzalia mutoto mwanaume. Musa akasema: “Nimekimbilia katika inchi ya kigeni”, kwa hiyo akamupa yule mutoto jina Gersomi. Nyuma ya muda murefu, mufalme wa Misri akakufa. Waisraeli wakaugua na kulia kutokana na hali yao ya utumwa na kilio chao kikamufikia Mungu juu. Mungu akasikia kilio chao, naye akakumbuka agano alilofanya na Abrahamu, Isaka, na Yakobo. Mungu akawaangalia Waisraeli, naye akatambua hali yao. Siku moja, Musa alikuwa anachunga kundi la kondoo la baba mukwe wake Yetro, kuhani wa Midiani. Musa akapeleka kundi lile upande wa magaribi wa jangwa, akafika kwenye mulima Horebu, mulima wa Mungu. Basi, malaika wa Yawe akamutokea katika mwali wa moto katikati ya kichaka. Musa akaangalia, akashangaa kuona kichaka kinawaka moto na wala hakiungui. Basi, akajisemesha: “Sasa nitazunguka nipate kuona jambo hili la ajabu, kichaka kuwaka moto na kisiungue!” Yawe alipoona kwamba Musa amegeuka kwa kuangalia kichaka, akamwita pale kutoka kichaka: “Musa! Musa!” Musa akaitika: “Niko hapa. Ninasikiliza!” Yawe akamwambia: “Usikuje karibu! Vua viatu vyako kwa sababu pahali unaposimama ni pahali patakatifu.” Kisha Mungu akamwambia: “Mimi ni Mungu wa baba yako, Mungu wa Abrahamu, Mungu wa Isaka, na Mungu wa Yakobo.” Musa akafunika uso wake kwa sababu aliogopa kumwangalia Mungu. Kisha Yawe akamwambia: “Nimeona mateso ya watu wangu wanaokuwa katika inchi ya Misri na nimesikia kilio chao kinachosababishwa na watesaji wao. Ninajua mateso yao, na hivyo, nimeshuka kusudi niwaokoe toka mikono ya Wamisri. Nitawatoa katika inchi na kuwapeleka katika inchi nzuri na kubwa, inchi inayotiririka maziwa na asali, inchi ya Wakanana, Wahiti, Waamori, Waperizi, Wahivi na Wayebusi. Hakika, kilio cha Waisraeli kimenifikia; nimeona jinsi Wamisri wanavyowatesa. Sasa, nitakutuma kwa mufalme wa Misri kusudi uwatoe watu wangu, watu wale wa Israeli, kutoka katika inchi ya Misri.” Lakini Musa akamwambia Mungu: “Mimi ni nani hata nimwendee mufalme wa Misri na kuwatoa Waisraeli katika inchi ya Misri?” Mungu akamwambia: “Hakika nitakuwa pamoja nawe. Utawatoa watu wa Israeli na kuja kuniabudu mimi Mungu juu ya mulima huu. Hicho kitakuwa kitambulisho kwamba ni mimi Mungu niliyekutuma wewe.” Halafu, Musa akamwambia Mungu: “Sasa, nikiwaendea Waisraeli na kuwaambia: ‘Mungu wa babu zenu amenituma kwenu’, nao wakiniuliza: ‘Jina lake ni nani?’, nitawaambia nini?” Mungu akamujibu: “Mimi Ndimi Ninayekuwa. Uwaambie watu wa Israeli kwamba: Yule anayeitwa Ndimi Ninayekuwa amekutuma kwao. Uwaambie Waisraeli kwamba: Yawe, Mungu wa babu zenu, Mungu wa Abrahamu, Mungu wa Isaka, na Mungu wa Yakobo, amekutuma kwao. Hili ndilo jina langu milele, na hivi ndivyo nitakavyokumbukwa katika vizazi vyote. Kwenda uwakusanye wazee wa Israeli na kuwaambia kwamba: Yawe, Mungu wa babu wao, Mungu wa Abrahamu, Mungu wa Isaka, na Mungu wa Yakobo, amekutokea na kusema: ‘Nimewachunguza ninyi na kuyaona mambo munayotendewa katika inchi ya Misri! Ninaahidi kwamba nitawatoa katika mateso yenu kule Misri na kuwapeleka katika inchi ya Wakanana, Wahiti, Waamori, Waperizi, Wahivi na Wayebusi. Nitawapeleka katika inchi inayotiririka maziwa na asali.’ “Wao watakusikiliza, nawe pamoja na wazee wa Waisraeli mutamwendea mufalme wa Misri na kumwambia: ‘Yawe, Mungu wa Waebrania, ametutokea. Sasa, uturuhusu tuende safari ya mwendo wa siku tatu katika jangwa, tumutolee Yawe, Mungu wetu, sadaka.’ Ninajua kwamba mufalme wa Misri hatawaacha muende asipolazimishwa kwa mukono wenye nguvu. Kwa hiyo nitaunyoosha mukono wangu na kupiga inchi ya Misri kwa maajabu ambayo nitayafanya kule. Kisha mufalme atawaacha muondoke. “Tena nitafanya Waisraeli wapate kukubaliwa mbele ya Wamisri na mutakapoondoka Misri, hamutatoka mikono mitupu. Kila mwanamuke Mwebrania atamwomba jirani yake Mumisri, au mugeni wake anayekuwa katika nyumba yake, amupe vyombo vya feza na zahabu pamoja na nguo. Hivyo mutawavalisha watoto wenu wanaume na wanawake. Ndivyo mutakavyowanyanganya Wamisri mali yao.” Musa akamwambia Mungu: “Lakini Waisraeli hawataniamini wala kunisikiliza. Watasema kwamba wewe Yawe haukunitokea.” Yawe akamwambia Musa: “Unashika nini katika mukono wako?” Musa akamwambia: “Fimbo.” Yawe akamwambia: “Uitupe chini.” Musa akatupa fimbo chini, nayo ikageuka kuwa nyoka. Musa akaikimbia. Lakini Yawe akamwambia Musa: “Nyoosha mukono wako, uikamate mukia!” Musa akanyoosha mukono wake, akaikamata na nyoka ikageuka tena kuwa fimbo katika mukono wake. Yawe akamwambia: “Hivyo Waisraeli watapata kuamini kwamba mimi Yawe, Mungu wa baba zao, Mungu wa Abrahamu, Mungu wa Isaka, na Mungu wa Yakobo, nimekutokea.” Tena, Yawe akamwambia Musa: “Ingiza mukono wako kwenye kifua chako.” Musa akafanya hivyo. Alipoutoa inje, ukakuwa na ukoma, mweupe kama teluji. Kisha Mungu akamwambia: “Ingiza tena mukono wako kwenye kifua chako!” Musa akaingiza mukono wake kwenye kifua. Alipoutoa inje, ukarudilia hali yake ya kawaida kama vile mwili wake unavyokuwa. Mungu akamwambia Musa: “Wasipokuamini au kusadiki kitambulisho cha kwanza, inawezekana wataamini kitambulisho cha pili. Lakini wasipoamini hata vitambulisho hivi viwili, au kuamini maneno yako, utachota maji ya muto Nili na kuyamwanga juu ya inchi kavu. Maji hayo yatakuwa damu juu ya inchi kavu.” Lakini Musa akamwambia Yawe: “Ewe Bwana wangu, mimi mutumishi wako sina ufundi wa kusema tangu zamani, hata kisha kusema nawe. Ulimi wangu ni muzito.” Halafu Yawe akamwuliza: “Ni nani aliyeumba kinywa cha mutu? Ni nani anayemufanya mutu kuwa bubu au kiziwi? Aone au akuwe kipofu? Si mimi Yawe? Basi, kwenda! Mimi nitaongoza kinywa chako na kukufundisha cha kusema.” Lakini Musa akasema: “Ee Bwana wangu, tafazali ninakusihi, umutume mutu mwingine.” Halafu hasira ya Mungu ikawaka juu ya Musa, akamwambia: “Si kuna ndugu yako Haruni ambaye ni Mulawi? Ninajua yeye anajua kusema vizuri. Tena anakuja kukutana nawe, na mara tu atakapokuona atafurahi ndani ya moyo. Wewe utaongea naye na kumwambia yote atakayosema. Mimi nitawasaidia na kuwafundisha mambo mutakayofanya. Haruni ataongea na Waisraeli kwa ajili yako. Yeye atakuwa musemaji wako, nawe utakuwa kama Mungu kwake. Utatwaa katika mukono wako fimbo hii ambayo utaitumia kufanya vile vitambulisho.” Musa akarudi kwa Yetro, baba mukwe wake, akamwambia: “Tafazali uniruhusu nirudie Misri kwa wandugu zangu, nione kama wangali wazima.” Yetro akamwambia: “Kwenda kwa amani.” Musa akiwa bado katika inchi ya Midiani, Yawe akamwambia: “Rudi Misri kwa sababu wale wote waliotaka kukuua wamekwisha kufa.” Basi, Musa akatwaa muke wake na watoto wake, akawapandisha juu ya punda, akaanza safari ya kurudi Misri. Katika mukono wake alishika ile fimbo aliyoamuriwa na Mungu aitwae. Yawe akamwambia Musa: “Utakapofika Misri, uhakikishe kwamba umetenda mbele ya mufalme wa Misri miujiza yote niliyokupa uwezo wa kuifanya. Lakini mimi nitafanya moyo wa mufalme wa Misri kuwa mugumu, naye hatawaachilia Waisraeli waondoke. Nawe utamwambia mufalme wa Misri kwamba Yawe anasema hivi: ‘Israeli ni mwana wangu, muzaliwa wangu wa kwanza. Nami ninakuambia: Umwache mwana wangu aondoke, kusudi anitumikie! Kama ukikataa kumwachilia aondoke, angalia nitamwua muzaliwa wako wa kwanza mwanaume.’ ” Akiwa bado katika njia kurudi Misri, Musa alikuwa pahali pa kulala pa wageni. Basi, Mungu akakutana naye na kutaka kumwua. Kwa hiyo Zipora akakimbia haraka, akatwaa jiwe kali, akakata govi la mwana wake na kumugusa nalo Musa kwenye miguu akisema: “Wewe ni bwana-arusi wa damu.” Kwa hiyo Yawe akamwacha Musa. Zipora alikuwa amesema: “Bwana-arusi wa damu”, kwa sababu ya kutahiri. Yawe akamwambia Haruni: “Kwenda katika jangwa ukutane na Musa.” Basi, Haruni akaenda, akakutana na Musa kwenye mulima wa Mungu, akamubusu. Naye Musa akamwambia Haruni maneno yote aliyoambiwa na Yawe ayaseme na vitambulisho vyote alivyoagizwa atende. Kisha Musa na Haruni wakaenda, wakawakusanya wazee wote wa Waisraeli. Haruni akawaambia maneno yote Yawe aliyokuwa amemwagiza Musa na kufanya vile vitambulisho mbele ya watu wote. Watu wakaamini. Na waliposikia kwamba Yawe amekuja kuwasaidia Waisraeli na kwamba ameyaona mateso yao, wote wakainamisha vichwa vyao na kumwabudu. Kisha, Musa na Haruni wakamwendea mufalme wa Misri, wakamwambia: “Yawe, Mungu wa Israeli anasema hivi: ‘Uwaache watu wangu waondoke, wanifanyie sikukuu katika jangwa.’ ” Lakini mufalme wa Misri akawauliza: “Ni nani yule Yawe, hata nimusikilize na kuwaacha Waisraeli waondoke? Mimi simujui yule Yawe, wala sitawaruhusu Waisraeli waondoke.” Musa na Haruni wakamwambia: “Mungu wa Waebrania amekutana nasi. Tunakusihi utuache tujiendee katika jangwa mwendo wa siku tatu tutoe sadaka kwa Yawe, Mungu wetu. Kama sivyo, yeye atatuua kwa ugonjwa mukali au kwa upanga.” Lakini mufalme wa Misri akawajibu: “Enyi Musa na Haruni, kwa nini munajaribu kuwatoa watu kwa kazi yao? Murudie kwa kazi yenu.” Tena mufalme akasema: “Hawa watu ni wengi nanyi munataka waache kufanya kazi!” Siku hiyohiyo mufalme wa Misri aliwaamuru wakubwa pamoja na wasimamizi, akasema: “Tangu leo musiwape watu hawa nyasi za kutengeneza matofali kama vile inavyokuwa kawaida. Wao wenyewe watakwenda kujitafutia. Lakini hesabu ya matofali yanayotengenezwa kila siku ikuwe ileile, wala kusipunguke hata tofali moja, kwa sababu watu hawa ni wavivu ndio maana wanapiga kelele na kusema: ‘Utuache tuende kutoa sadaka kwa Mungu wetu.’ Muwazidishie watu hawa kazi ngumu kusudi watoke jasho na kuacha kusema maneno ya uongo.” Basi, wakubwa na wasimamizi wa watu wakatoka na kuwaambia watu: “Mufalme wa Misri anasema hivi: ‘Sitawapa nyasi. Muende ninyi wenyewe mutafute popote mutakapoweza kuzipata, na wala kazi yenu haitapunguzwa hata kidogo.’ ” Basi, watu wote wakatawanyika kila pahali katika inchi ya Misri wakitafuta nyasi za kutengeneza matofali. Nao wakubwa wakakazana wakisema: “Mutimize kazi yenu ya kila siku kama mbele mulipoletewa nyasi.” Wakubwa wa Wamisri wakawapiga wasimamizi wa Waisraeli waliochaguliwa kusimamia kazi wakisema: “Kwa nini hamutimizi kazi yenu na kufikisha hesabu ileile ya matofali kama mbele?” Halafu wasimamizi wa Waisraeli wakamwendea mufalme, wakamulilia wakisema: “Kwa nini unatutendea hivi sisi watumishi wako? Hatupewi tena nyasi wakati tunalazimishwa kufyatua matofali. Tena sisi watumishi wako tunapigwa, ingawa kosa ni la watu wako.” Lakini mufalme wa Misri akasema: “Wavivu ninyi! Ninyi ni wavivu, ndiyo maana munasema: ‘Utuache tuende kutoa sadaka kwa Yawe’. Muende sasa mufanye kazi; maana hamutapewa nyasi na mutafyatua hesabu ileile ya matofali.” Basi, wale wasimamizi wa Waisraeli sasa walijiona kuwa katika taabu, maana waliambiwa: “Hamutapunguza hata kidogo hesabu ya matofali ya kila siku.” Walipoondoka kwa mufalme, wakakutana na Musa na Haruni ambao walikuwa wanawangojea. Basi, wakawaambia Musa na Haruni: “Yawe aone jambo hili na kuwahukumu ninyi kwa sababu mumetufanya sisi kuwa chukizo kwa mufalme wa Misri na wakubwa wake. Ninyi mumewapa sababu ya kutuua.” Kisha Musa akamugeukia tena Yawe, akasema: “Ee Yawe, kwa nini unawatendea watu hawa uovu? Kwa nini hata ulinituma? Tangu nilipokwenda na kuongea na mufalme wa Misri kwa jina lako, yeye amewatendea watu hawa uovu. Wewe haujafanya lolote kwa kuwakomboa watu wako.” Lakini Yawe akamujibu Musa: “Sasa utaona jinsi nitakavyomutendea mufalme wa Misri. Kwa nguvu atalazimishwa kuwaacha watu wangu watoke. Kwa nguvu atawafukuza waondoke katika inchi yake.” Mungu akamwambia Musa: “Mimi ni Yawe. Nilimutokea Abrahamu, Isaka, na Yakobo nikijulikana kama Mungu Mwenye Nguvu, ingawa sikuwajulisha jina langu, Yawe. Tena nilifanya agano nao kwamba nitawapa inchi ya Kanana ambako waliishi kama wageni. Zaidi ya hayo, nimesikia kilio cha Waisraeli ambao wamelazimishwa kufanya kazi za kitumwa na Wamisri, nikalikumbuka agano langu. Kwa hiyo, uwaambie Waisraeli hivi: ‘Mimi ni Yawe! Mimi nitawatoa katika nira mulizowekewa na Wamisri. Nitawaokoa toka utumwa wenu. Nitanyoosha mukono wangu wenye nguvu na kuwaazibu vikali Wamisri na kuwakomboa ninyi. Nitawafanya kuwa watu wangu, nami nitakuwa Mungu wenu. Ninyi mutatambua kwamba mimi ni Yawe, Mungu wenu, niliyewatoa katika nira za Wamisri. Nami nitawapeleka katika inchi ile niliyoapa kumupa Abrahamu, Isaka, na Yakobo. Nitawapa inchi hiyo ikuwe yenu. Mimi ni Yawe.’ ” Musa akawaelezea Waisraeli maneno hayo. Lakini wao hawakumusikiliza kwa sababu walikuwa wamekufa moyo kutokana na utumwa mukali. Kisha Yawe akamwambia Musa: “Kwenda kwa mufalme wa Misri, umwambie awaache Waisraeli waondoke katika inchi yake.” Lakini Musa akamwambia Yawe: “Angalia, Waisraeli hawanisikilizi mimi. Namna gani mufalme wa Misri atanisikia! Tena mimi ni mutu asiyekuwa na ujuzi wa kuongea!” Lakini Yawe akaongea na Musa na Haruni, akawaagiza waende kwa mufalme wa Misri, na kuwatoa Waisraeli kutoka inchi ya Misri. Haya ndiyo majina ya wakubwa wa jamaa za Waisraeli. Wana wa Rubeni, muzaliwa wa kwanza wa Israeli: Hanoki, Palu, Hesironi na Karmi. Hao walikuwa babu za jamaa za Rubeni. Wana wa Simeoni walikuwa: Yemueli, Yamini, Ohadi, Yakini, Sohari na Sauli. Huyu wa mwisho alikuwa mutoto wa mwanamuke wa Kanana. Hao walikuwa babu za jamaa za Simeoni. Sasa haya ni majina ya wana wa Lawi na wazao wao: Gersoni, Kohati na Merari. Lawi aliishi miaka mia moja makumi tatu na saba. Wana wa Gersoni walikuwa: Libuni na Simei. Hao walikuwa babu za jamaa zao. Wana wa Kohati walikuwa: Amuramu, Izihari, Hebroni na Uzieli. Kohati aliishi miaka mia moja makuni tatu na mitatu. Wana wa Merari walikuwa: Mali na Musi. Hao ndio babu za jamaa za Walawi. Amuramu alimwoa Yokebedi, shangazi yake, naye akamuzalia Haruni na Musa. Amuramu aliishi miaka mia moja makumi tatu na saba. Na wana wa Izihari walikuwa: Kora, Nefegi na Zikiri. Wana wa Uzieli walikuwa: Misaeli, Elisafani na Sitri. Haruni alimwoa Eliseba, binti ya Aminadabu, dada ya Nasoni; naye akamuzalia Nadabu, Abihu, Eleazari na Itamari. Nao wana wa Kora walikuwa: Asiri, Elkana na Abiasafu, ambao walikuwa babu za jamaa za Kora. Eleazari mwana wa Haruni, alimwoa mumoja wa wabinti za Putieli, naye akamuzalia Finehasi. Hawa ndio waliokuwa wakubwa wa jamaa za Lawi. Haruni na Musa ndio walioambiwa na Yawe: “Mutoe watu wa Israeli kutoka inchi ya Misri, vikundi kwa vikundi.” Ndio haohao Musa na Haruni walioongea na mufalme wa Misri, juu ya kuwatoa Waisraeli kutoka inchi ya Misri. Siku ile Yawe alipoongea na Musa katika inchi ya Misri, alimwambia: “Mimi ni Yawe. Umwambie mufalme wa Misri maneno yote ninayokuambia.” Lakini Musa akamwambia Yawe: “Mimi sina ujuzi wa kuongea. Mufalme wa Misri atanisikiliza namna gani?” Yawe akamwambia Musa: “Mimi ninakufanya kuwa kama mungu kwa mufalme wa Misri, naye ndugu yako Haruni atakuwa nabii wako. Utamwambia ndugu yako Haruni mambo yote nitakayokujulisha. Naye Haruni ndugu yako, atamwambia mufalme wa Misri awaache Waisraeli watoke katika inchi yake. Lakini nitafanya moyo wa mufalme kuwa mugumu. Na hata kama nitazidisha vitambulisho na maajabu yangu katika inchi ya Misri, Mufalme wa Misri hatakusikiliza. Na hapo nitanyoosha mukono wangu wenye nguvu na kuazibu vikali inchi ya Misri na kuwatoa watu wangu, makabila ya Israeli, kutoka Misri. Nitafanya hivyo kwa matendo makubwa ya hukumu juu ya Misri, wakati nitakaponyoosha mukono wangu juu ya inchi ya Misri na kuwatoa Waisraeli kati yao. Halafu Wamisri watatambua kwamba mimi ni Yawe.” Basi, Musa na Haruni wakafanya hivyo. Hakika, walifanya kama vile Yawe alivyowaamuru. Musa alikuwa na umri wa miaka makumi nane, na Haruni alikuwa na umri wa miaka makumi nane na mitatu wakati ule walipoongea na mufalme wa Misri. Yawe akamwambia Musa na Haruni: “Mufalme wa Misri atakapowaambia muhakikishe jambo lile kwa kutenda miujiza, wewe utamwambia Haruni atwae fimbo yake, aitupe mbele ya mufalme, nayo itakuwa nyoka.” Basi, Musa na Haruni wakamwendea mufalme wa Misri na kufanya kama vile walivyoamuriwa na Yawe. Haruni akatupa fimbo yake chini mbele ya mufalme na wakubwa wake, nayo ikakuwa nyoka. Lakini, mufalme wa Misri akawaita wenye hekima wake na wachawi. Wale wachawi wa Misri wakafanya vile vile kwa uchawi wao. Kila mumoja akatupa fimbo yake chini, ikakuwa nyoka. Lakini fimbo ya Haruni ikameza fimbo zao. Hata hivyo, moyo wa mufalme ulibaki tu kuwa mugumu, wala hakuwasikiliza. Ikakuwa kama vile Yawe alivyosema. Kisha Yawe akamwambia Musa: “Moyo wa mufalme wa Misri umekuwa mugumu. Anakataa kuwaacha Waisraeli waondoke. Basi, kwenda ukutane naye kesho asubui, wakati anapokwenda kwenye muto Nili. Umungojee kando ya muto. Utwae katika mukono wako ile fimbo iliyogeuka kuwa nyoka. Kisha umwambie hivi: Yawe, Mungu wa Waebrania, amenituma kwako, naye anasema hivi: ‘Uwaache watu wangu waende zao kusudi wanitumikie katika jangwa. Lakini mpaka sasa wewe haupendi kutii. Basi, Yawe anasema kwamba sasa utamutambua yeye ni nani. Nitayapiga maji ya muto Nili kwa fimbo hii na maji yote yatageuka kuwa damu. Samaki wanaokuwa ndani ya muto Nili watakufa, muto wote utanuka vibaya, na Wamisri watachukia kabisa kunywa maji yake.’ ” Yawe akamwambia Musa: “Umwambie Haruni atwae fimbo yake na kuiinua juu ya maji ya Misri, juu ya mito yote, mifereji, visima na maji yao yote, nayo yatakuwa damu. Kutakuwa damu katika inchi yote, na hata katika vyombo vyote vya muti na vya mawe.” Musa na Haruni wakafanya kama vile Yawe alivyowaamuru. Haruni akainua fimbo yake juu mbele ya mufalme wa Misri na wakubwa wake, akayapiga maji ya muto Nili, na maji yote katika muto yakageuka kuwa damu. Samaki wakakufa, muto ukanuka vibaya sana hata Wamisri hawakuweza kunywa maji yake. Inchi nzima ikajaa damu. Lakini wachawi wa Misri kwa kutumia uchawi wao wakafanya vivyo hivyo. Kwa hiyo moyo wa mufalme wa Misri ukabaki kuwa mugumu, naye hakuwasikiliza Musa na Haruni. Ikakuwa kama vile Yawe alivyokuwa amesema. Basi, mufalme wa Misri akarudi katika nyumba yake na hata yale yaliyotokea hakuyajali. Wamisri wote wakachimbachimba kandokando ya muto Nili kusudi wapate maji ya kunywa, maana hawakuweza kunywa maji ya muto ule. Pigo hilo la muto Nili lilidumu siku saba. Kisha Yawe akamwambia Musa: “Kwenda kwa mufalme wa Misri umwambie Yawe anasema hivi: Uwaache watu wangu waondoke kusudi wanitumikie. Lakini ukikataa kuwaacha waondoke, basi, nitapiga inchi yako yote kwa kuiletea vyura. Muto Nili utajaa vyura, nao wataingia mpaka ndani ya nyumba yako, chumba chako cha kulala, juu ya kitanda chako, na katika nyumba za watumishi wako na watu wako. Vyura hao wataingia katika mafika yenu na vyombo vyenu vya kufinyangia unga. Vyura watapanda juu ya mwili wako, miili ya watu wako na watumishi wenu!” Yawe akamwambia Musa: “Umwambie Haruni anyooshe mukono wake na kuinua fimbo yake juu ya mito, juu ya mifereji na visima, nao vyura watatokea na kuenea kila pahali katika inchi ya Misri.” Basi, Haruni akainua fimbo yake juu ya maji yote. Vyura wakatokea na kufunika inchi nzima ya Misri. Lakini wachawi wa Misri kwa uchawi wao vilevile wakaleta vyura katika inchi ya Misri. Kisha mufalme wa Misri akamwita Musa na Haruni, akawaambia: “Musihi Yawe, kusudi aniondolee mimi na watu wangu vyura hawa, nami nitawaacha Waisraeli wajiendee na kutoa sadaka kwa Yawe.” Musa akamujibu mufalme wa Misri: “Basi! Unaweza kutaja wakati unaotaka nikuombee kwa Mungu, niwaombee wakubwa wako na watu wako. Nitamwomba awaangamize vyura hawa wanaokuwa katika nyumba zenu. Watabaki tu katika muto Nili!” Mufalme wa Misri akamwambia: “Kesho.” Musa akasema: “Nitafanya kama vile unavyosema, kusudi ujue kwamba hakuna yeyote anayelingana na Yawe, Mungu wetu. Vyura wataondoka kwako, na kwenye nyumba zenu, kwa wakubwa wako na kwa watu wako. Watabaki tu katika muto Nili.” Basi, Musa na Haruni wakaondoka kwa nyumba ya mufalme wa Misri na Musa akamulilia Yawe amwondolee mufalme vyura wale aliomuletea. Yawe akafanya kama vile Musa alivyomwomba. Vyura wakakufa katika nyumba, viwanja na kwenye baraza za nyumba na katika mashamba. Watu wakawakusanya vyura wale malundomalundo. Inchi nzima ikanuka. Lakini mufalme wa Misri alipoona kwamba inchi imepata utulivu, akakuwa na moyo mugumu tena, wala hakusikiliza Musa na Haruni, kama vile Yawe alivyokuwa amesema. Kisha, Yawe akamwambia Musa: “Umwambie Haruni ainue fimbo yake na kupiga mavumbi, nayo yatageuka kuwa chawa katika inchi yote ya Misri.” Musa na Haruni wakafanya hivyo. Haruni akainua fimbo yake na kupiga mavumbi, nayo yakageuka kuwa chawa nao wakakuwa juu ya watu na nyama. Mavumbi yote katika inchi yote ya Misri yakageuka kuwa chawa. Wachawi wa Misri, kwa uchawi wao, wakajaribu kuyageuza mavumbi yakuwe chawa, lakini hawakuweza. Chawa wale wakaenea juu ya watu na nyama. Wale wachawi wakamwambia mufalme wa Misri: “Hii ni kazi ya mukono wa Mungu.” Lakini moyo wa mufalme ukaendelea kuwa mugumu, wala hakuwasikiliza Musa na Haruni. Ikakuwa kama vile Yawe alivyokuwa amesema. Kisha Yawe akamwambia Musa: “Kesho amuka asubui mapema umwendee mufalme wa Misri wakati anapokwenda kwenye muto umwambie: ‘Yawe anasema hivi: Uwaache watu wangu waondoke kusudi wanitumikie. Kama ukikataa kuwaacha waondoke, basi, nitakuletea makundi ya mainzi, wewe, wakubwa wako na watu wako wote. Wataingia kwenye nyumba zenu na nyumba zote za Wamisri zitajaa makundi ya mainzi na inchi yote ya Misri vilevile. Lakini siku hiyo sehemu ya Goseni watu wangu wanakoishi nitaikinga. Kule mainzi wale hawatakuwa. Kwa hiyo utatambua kwamba mimi Yawe ninatenda mambo katika inchi yako. Nitakinga watu wangu na mambo yatakayowapata watu wako. Mambo hayo yatafanyika kesho.’ ” Yawe akafanya kama vile alivyosema. Makundi makubwa ya mainzi yakashambulia nyumba ya mufalme wa Misri, nyumba za wakubwa wake na inchi nzima ya Misri. Inchi nzima ya Misri ikaharibiwa na mainzi wale. Halafu mufalme wa Misri akawaita Musa na Haruni, akawaambia: “Munaweza kwenda kutoa sadaka kwa Mungu wenu, lakini ikuwe humuhumu katika inchi ya Misri.” Lakini Musa akamujibu: “Hapana! Haifai kufanya hivyo, maana sadaka tutakazomutolea Yawe, Mungu wetu, zitawachukiza Wamisri. Wamisri wakituona tunatoa sadaka ambazo ni chukizo kwao, si watatupiga mawe? Tusafiri mwendo wa siku tatu katika jangwa tumutolee Yawe, Mungu wetu, sadaka kama vile atakavyotuamuru.” Basi, mufalme wa Misri akasema: “Nitawaacha mujiendee kutoa sadaka kwa Yawe, Mungu wenu, katika jangwa. Lakini musiende mbali sana. Muniombee mimi.” Musa akamujibu: “Mara tu nitakapokuacha, kesho nitamwomba Yawe makundi haya ya mainzi yatoweke kwako wewe mufalme, wakubwa wako na watu wako. Lakini wewe usitudanganye tena kwa kukataa kuwaacha watu kwenda kutoa sadaka kwa Yawe.” Basi, Musa akaondoka kwa nyumba ya mufalme wa Misri, akamwomba Yawe. Yawe akafanya kama vile Musa alivyomwomba. Wale mainzi wakatoweka kutoka kwa mufalme wa Misri, wakubwa wake na watu wake, wala hakukubaki hata mumoja. Lakini hata mara hii mufalme wa Misri akafanya moyo wake kuwa magumu, wala hakuwaruhusu Waisraeli kuondoka. Kisha Yawe akamwambia Musa: “Kwenda kwa mufalme wa Misri umwambie kwamba mimi Yawe, Mungu wa Waebrania, ninasema hivi: ‘Uwaache watu wangu waondoke kusudi wanitumikie. Kama ukikataa kuwaacha waondoke na ukiendelea kuwashikilia, nitanyoosha mukono wangu na kuleta ugonjwa mukali sana juu ya nyama wenu wote: ngombe, farasi, punda, ngamia, mbuzi na kondoo. Na nitaitenganisha mifugo ya Waisraeli na mifugo ya Wamisri kusudi nyama hata mumoja wa Waisraeli asikufe.’ ” Tena, Yawe akaweka wakati akisema: “Kesho mimi Yawe nitatimiza jambo hilo katika inchi ya Misri.” Kesho yake Yawe akafanya kile alichosema. Mifugo yote ya Wamisri ikakufa, lakini hakuna nyama hata mumoja wa Waisraeli aliyekufa. Mufalme wa Misri akauliza habari juu ya nyama wa Waisraeli. Wakamwambia kwamba hakuna nyama wao hata mumoja aliyekufa. Hata hivyo, Mufalme akabaki akifanya moyo wake kuwa mugumu, wala hakuwaruhusu Waisraeli waondoke. Yawe akamwambia Musa na Haruni: “Mutwae kila mumoja wenu vitanga vya majivu ya furu, kisha Musa ayarushe juu katika hewa mbele ya mufalme wa Misri. Majivu hayo yatakuwa vumbi nyembamba itakayoenea juu ya inchi yote ya Misri. Yatasababisha majipu yatakayopasuka na kuwa vidonda kwa watu na nyama kila pahali katika inchi ya Misri.” Basi, wakatwaa majivu kutoka kwenye furu, wakamwendea mufalme wa Misri, naye Musa akayarusha juu katika hewa. Watu na nyama wakapatwa na majipu. Hata wale wachawi hawakuweza kujitokeza, maana wao pamoja na Wamisri wote vilevile walipatwa na majipu hayo. Lakini Yawe akafanya moyo wa mufalme wa Misri kuwa mugumu, naye hakuwasikiliza kama vile Yawe alivyomwambia Musa. Kisha, Yawe akamwambia Musa: “Kesho, amuka asubui mapema umwendee mufalme wa Misri, umwambie kwamba mimi Yawe, Mungu wa Waebrania, ninasema hivi: ‘Uwaache watu wangu waondoke kusudi wanitumikie. Maana mara hii, wewe mwenyewe, wakubwa wako na watu wako mutapatwa na mapigo yangu makali. Nawe utatambua kwamba hakuna yeyote katika dunia anayekuwa kama mimi. Ningalikwisha kukuangamiza wewe na watu wako kwa ugonjwa mukali, nanyi mungalikuwa mumekwisha kuangamia. Lakini nimewaacha muishi kwa kuonyesha uwezo wangu. Kwa hiyo dunia yote itatambua kwamba mimi ni nani. Lakini ungali unaonyesha kiburi juu ya watu wangu, wala hauwaachi waondoke. Kwa hiyo kesho, wakati kama huu, nitaleta mvua kubwa ya mawe ambayo haijatokea katika inchi ya Misri, tangu mwanzo wake mpaka leo. Kwa hiyo agiza kwamba mifugo yako na chochote kinachokuwa kule katika mashamba viwekwe pahali salama. Mvua ya mawe itamunyeshea kila mutu na nyama anayekuwa katika shamba na ambaye hayuko ndani ya nyumba. Wote watakufa.’ ” Wakubwa wamoja wa mufalme wa Misri wakaogopa maneno hayo ya Yawe, wakawapeleka watumwa na nyama wao ndani ya nyumba pahali pa usalama. Lakini yule ambaye hakujali neno la Yawe aliwaacha watumwa wake na nyama wake katika mashamba. Kisha, Yawe akamwambia Musa: “Nyoosha mukono wako juu mbinguni, kusudi mvua ya mawe inyeshe kila pahali katika inchi ya Misri. Imunyeshee mutu, nyama na kila mumea katika shamba.” Basi, Musa akainua fimbo yake kuelekea mbinguni. Naye Yawe akaleta mvua ya mawe na ngurumo, umeme ukapiga inchi. Yawe alinyesha mvua ya mawe juu ya inchi ya Misri, mvua kubwa ya mawe iliyofuatana na mufululizo wa umeme, ambayo hakuna mwanainchi yeyote wa Misri aliyepata hata kidogo kushuhudia mbele. Mvua hiyo ya mawe ilivunjavunja kila kitu katika mashamba na kila pahali katika inchi ya Misri, nyama na watu. Mawe ya mvua yakavunjavunja mimea yote na miti katika mashamba. Mvua ya mawe haikunyesha tu katika inchi ya Goseni ambako Waisraeli walikuwa wanakaa. Basi, mufalme wa Misri akaagiza Musa na Haruni waitwe, akawaambia: “Mara hii nimetenda zambi. Yawe ana haki na mimi na watu wangu tumekosa. Mumwombe Yawe maana ngurumo hii na mvua ya mawe vimezidi. Mimi nitawaacha muondoke na wala hamutabakia tena.” Musa akamwambia: “Mara tu nitakapotoka inje ya muji nitainua mikono na kumwomba Yawe. Ngurumo itakoma na hakutakuwa mvua ya mawe tena kusudi utambue kwamba dunia ni ya Yawe. Lakini ninajua kwamba wewe na wakubwa wako mungali hamumwogopi Yawe Mungu.” (Kitani na mimea ya shayiri vyote vilikuwa vimeharibiwa, kwa sababu shayiri ilikuwa na masuke na kitani ilikuwa imechanua maua. Lakini ngano na jamii nyingine ya ngano havikuharibiwa kwa sababu hiyo inachelewa kukomaa). Basi, Musa akaondoka katika nyumba ya mufalme, akatoka inje ya muji. Kisha akainua mikono yake kumwomba Yawe. Ngurumo na mvua ya mawe vikakoma, mvua ikaacha kunyesha katika dunia. Lakini mufalme wa Misri alipoona kwamba mvua ya mawe na ngurumo vimekoma, akarudilia zambi yake tena. Akafanya moyo wake kuwa mugumu, yeye pamoja na wakubwa wake. Basi, kama vile Yawe alivyomwambia Musa, moyo wa mufalme wa Misri ulikuwa mugumu, yeye na wakubwa wake, akakataa kuwaruhusu Waisraeli waondoke. Yawe akamwambia Musa: “Kwenda kwa mufalme wa Misri. Mimi nimefanya moyo wake kuwa mugumu na wa wakubwa wake kusudi nipate kuonyesha vitambulisho hivi kati yao, na ninyi mupate kuwaelezea watoto wenu na wajukuu wenu jinsi nilivyowachekelea Wamisri kwa kuonyesha vitambulisho vile kati yao. Hivyo mutatambua kwamba mimi ni Yawe.” Basi, Musa na Haruni wakamwendea mufalme wa Misri na kumwambia: “Yawe, Mungu wa Waebrania, anasema hivi: ‘Mpaka wakati gani utakataa kujinyenyekeza mbele yangu? Uwaache watu wangu waondoke kusudi wanitumikie. Ukikataa kuwaacha watu wangu waondoke, basi, kesho nitaleta nzige washambulie inchi yako. Inchi yote ya Misri itakuwa giza kwa sababu ya nzige wale. Watakula kila kitu kilichobaki nyuma ya ile mvua ya mawe. Vilevile hawataacha chochote juu ya miti inayoota katika mashamba. Nzige wale watajaa katika nyumba zako, nyumba za wakubwa wako na za Wamisri wote. Watakuwa wengi kiasi ambacho hata wazee wenu hawajapata kuona tangu walipozaliwa, mpaka leo.’ ” Basi, Musa akatoka kwa mufalme wa Misri. Viongozi wa mufalme wakamwuliza: “Mutu huyu atatusumbua mpaka wakati gani? Uwaache watu hawa wajiendee wamutumikie Yawe, Mungu wao. Haujali kwamba inchi ya Misri inaangamia?” Hapo, Musa na Haruni wakaitwa warudi kwa mufalme wa Misri, naye akawaambia: “Muende mumutumikie Yawe, Mungu wenu. Lakini, ninauliza, ni nani watakaokwenda pamoja nanyi?” Musa akamujibu: “Kila mutu, vijana na wazee, tutaondoka na watoto wetu wanaume na wanawake, kondoo na mbuzi wetu na ngombe. Kwa maana tunapaswa kumufanyia Yawe sikukuu.” Mufalme wa Misri akawaambia: “Basi, Yawe akuwe pamoja nanyi kama nitawaruhusu mujiendee na watoto wenu. Ni wazi kwamba muko na nia mbaya ndani ya moyo wenu. Haitakuwa vile! Ni wanaume tu watakaokwenda kumutumikia Yawe, maana hilo ndilo munalotaka.” Halafu Musa na Haruni wakafukuzwa toka mbele ya mufalme. Yawe akamwambia Musa: “Nyoosha mukono wako juu ya inchi ya Misri, nzige watokee kusudi waingie na kula mimea yote katika inchi na vyote vilivyoachwa na ile mvua ya mawe.” Basi, Musa akainua fimbo yake juu ya inchi ya Misri. Yawe akaleta upepo toka upande wa mashariki, ukavuma juu ya inchi muchana kutwa na usiku kucha. Kulipokucha, ule upepo ukaleta nzige. Wale nzige wakaenea kila pahali katika inchi ya Misri, wakatua juu ya inchi yote. Nzige wale walikuwa kundi kubwa sana, kiasi ambacho hakijapata kutokea wala hakitatokea tena. Walifunika inchi yote ya Misri, hata inchi ikaonekana kuwa giza. Walikula mimea yote na matunda yote yaliyobaki wakati wa ile mvua ya mawe. Hakuna hata jani moja lililobakia katika inchi. Hakuna jani lolote lililobakia juu ya miti wala mimea popote katika inchi yote ya Misri. Hapo mufalme wa Misri akaita Musa na Haruni kwa haraka, akawaambia: “Nimetenda zambi mbele ya Yawe, Mungu wenu, na mbele yenu. Kwa hiyo sasa ninawasihi munisamehe zambi yangu mara hii, muniombee kwa Yawe, Mungu wenu, aniondolee kifo hiki.” Basi, Musa akaondoka kwa mufalme, akaenda kumwomba Yawe. Naye Yawe akaleta upepo mukali toka upande wa magaribi, ukawainua wale nzige na kuwasukumia kwenye bahari Nyekundu. Hakuna hata nzige mumoja aliyebaki katika inchi nzima ya Misri. Lakini Yawe akafanya moyo wa mufalme kuwa mugumu, naye hakuwaachilia Waisraeli waondoke. Yawe akamwambia Musa: “Nyoosha mukono wako juu mbinguni kusudi giza nzito litokee katika inchi ya Misri, giza nzito sana ambalo mutu ataweza kulipapasa.” Basi, Musa akanyoosha mukono wake juu mbinguni, kukakuwa giza nzito katika inchi yote ya Misri kwa muda wa siku tatu. Watu hawakuweza kuonana wala kuondoka pahali walipokuwa kwa muda ule wa siku tatu. Lakini Waisraeli wote walikuwa na mwangaza kule Goseni walikokuwa wanakaa. Kisha, mufalme wa Misri akamwita Musa, akamwambia: “Mwende mumutumikie Yawe. Watoto wenu vilevile wanaweza kwenda pamoja nanyi. Lakini kondoo na mbuzi, na ngombe wenu wabaki.” Lakini Musa akamwambia: “Unapaswa kuturuhusu kutwaa nyama wa matoleo na sadaka za kuteketezwa kwa kumutolea Yawe, Mungu wetu. Ngombe wetu tunapaswa vilevile kuwapeleka wala hakuna hata nyama mumoja atakayebaki nyuma. Kwa sababu kutoka katika mifugo yetu wenyewe, tutamutumikia Yawe, Mungu wetu, wala sisi hatujui ni nyama gani tutakayemutolea Yawe sadaka mpaka tutakapofika kule.” Lakini Yawe akaufanya moyo wa mufalme wa Misri kuwa mugumu, akakataa kuwaachilia Waisraeli waondoke. Mufalme akamwambia Musa: “Toka mbele yangu! Ufanye angalisho sana! Usikuje kuniona tena, maana siku utakapokuja tena mbele yangu, utakufa!” Musa naye akamwambia: “Sawa! Kama vile ulivyosema sitakuja kukuona tena.” Yawe akamwambia Musa: “Kungali bado pigo moja nitakalomuletea mufalme wa Misri na inchi ya Misri. Kisha atawaacha muondoke hapa. Naye atakapowaacha muondoke, atawafukuza kwa lote. Uwaambie Waisraeli sasa wasikie vizuri kwamba kila mumoja wao, mwanaume na mwanamuke, anapaswa kumwomba jirani yake vyombo vya feza na zahabu.” Yawe akawafanya Waisraeli wapate kukubaliwa mbele ya Wamisri. Tena, Musa mwenyewe akakuwa mutu mukubwa sana katika inchi ya Misri na mbele ya wakubwa na mufalme na watu wote. Musa akamwambia mufalme wa Misri: “Yawe anasema hivi: ‘Katikati ya usiku wa leo, nitapitia katikati ya inchi ya Misri. Nitakapopita, kila muzaliwa wa kwanza katika inchi ya Misri atakufa, kuanzia muzaliwa wa kwanza wako wewe mufalme wa Misri ambaye ni murizi wako, mpaka muzaliwa wa kwanza wa mujakazi anayesaga ngano kwa jiwe. Hata wazaliwa wa kwanza wa mifugo nao wote watakufa. Kutakuwa kilio kikubwa katika inchi yote ya Misri, kilio ambacho hakijapata kutokea, wala hakitatokea tena. Lakini kati ya Waisraeli hakuna hata imbwa atakayemufokea mutu wala nyama kusudi upate kutambua kwamba mimi Yawe ninaweka tofauti kati ya Waisraeli na Wamisri.’ ” Musa akamalizia kwa kumwambia mufalme: “Watumishi wako hawa watanifikia na kuinama mbele yangu kwa heshima, wakinisihi niondoke katika inchi ya Misri, mimi pamoja na watu wote wanaonifuata. Nyuma ya hayo, nitaondoka.” Kisha Musa, akiwa amekasirika, akaondoka kwa mufalme wa Misri. Yawe akamwambia Musa: “Mufalme wa Misri hatakusikiliza, kusudi maajabu yangu yapate kuongezeka katika inchi ya Misri.” Basi, Musa na Haruni walifanya maajabu hayo yote mbele ya mufalme wa Misri. Lakini Yawe alifanya moyo wa mufalme kuwa mugumu, akakataa kuwaruhusu Waisraeli waondoke katika inchi yake. Yawe akamwambia Musa na Haruni, walipokuwa wangali katika inchi ya Misri: “Mwezi huu utakuwa kwenu mwezi wa kwanza wa mwaka. Muwaambie Waisraeli wote pamoja kwamba katika siku ya kumi ya mwezi huu, mutatwaa mwana-kondoo mumoja kwa kila jamaa moja. Kama jamaa moja ni ndogo sana hata isiweze kumaliza kondoo mumoja, itashirikiana na jamaa jirani kadiri ya hesabu ya watu wake. Kisha watachagua nyama ambaye kila mutu ataweza kula. Mwana-kondoo yule asikuwe na kilema chochote, akuwe dume wa mwaka mumoja. Anaweza kuwa mwana-kondoo au mwana-mbuzi. Mutamuweka nyama yule mpaka siku ya kumi na ine ya mwezi huu. Siku hiyo, Waisraeli watawachinja nyama wale wakati wa magaribi. Kisha, watatwaa damu ya wale nyama na kuipakaa juu ya miimo na vizingiti vya kila nyumba watakamokulia nyama wale. Watakula nyama hiyo usiku uleule kisha kuichoma. Wataikula pamoja na mukate usiotiwa chachu na mboga chungu za majani. Imekatazwa kuikula ikiwa mbichi au imetokoteshwa kwa maji, lakini inapaswa kuchomwa yote, pamoja na kichwa, miguu na nyama zake za ndani. Vilevile musiache nyama yoyote mpaka asubui. Nyama yoyote itakayobaki mpaka asubui mutaiteketeza kwa moto. Na hivi ndivyo mutakavyokula nyama yule: mutakuwa tayari kwa kusafiri, na kuvaa viatu na kuwa na fimbo zenu katika mikono. Tena mutamukula kwa haraka. Hiyo ni Pasaka ya Yawe. “Usiku ule, nitapita katika inchi ya Misri na kuwaua wazaliwa wa kwanza wa Misri, watu na nyama. Nitaiazibu miungu yote ya Misri. Mimi ni Yawe. Basi, ile damu itakuwa kitambulisho chenu cha kuonyesha nyumba mutakamokuwa. Nami nitakapoiona ile damu, nitawapita ninyi, hamutapatwa na hasara yoyote wakati nitakapoipiga inchi ya Misri. Vizazi hata vizazi mutakumbuka tukio hilo kwa sikukuu kubwa kwa heshima yangu mimi Yawe. Hilo litakuwa agizo la milele kwenu.” Yawe akaendelea kusema: “Kwa muda wa siku saba, mutakula mikate isiyotiwa chachu. Siku ya kwanza ya siku hizo saba, mutaondoa chachu katika nyumba zenu. Mutu yeyote akikula kitu kilichotiwa chachu katika muda ule wa siku saba, anapaswa kuondolewa kati ya Waisraeli. Siku ya kwanza na siku ya saba mutakuwa na mukutano mutakatifu. Katika siku hizo mbili hamutaruhusiwa kufanya kazi yoyote isipokuwa kazi ya lazima ya kutayarisha chakula. Mutashika sikukuu hii ya Mikate Isiyotiwa Chachu kama ukumbusho wa siku nilipowatoa ninyi vikundi vya Israeli kutoka Misri. Sikukuu hiyo itashikwa na vizazi vyenu vyote vinavyokuja, kama agizo la milele. Basi, mutakula mikate isiyotiwa chachu kuanzia magaribi ya siku ya kumi na ine ya mwezi wa kwanza, mpaka magaribi ya siku ya makumi mbili na moja ya mwezi uleule wa kwanza. Katika siku hizo saba, musikuwe na chachu yoyote katika nyumba zenu. Mutu yeyote, akuwe mugeni au mwenyeji, akikula kitu kilichotiwa chachu, ataondolewa katika kusanyiko la Waisraeli. Popote pale munapoishi, hamutakula chochote kilichotiwa chachu. Munapaswa kula mikate isiyotiwa chachu.” Basi, Musa akawaita wazee wote wa Waisraeli, akawaambia: “Muchague kila mumoja wenu, kulingana na jamaa yake, mwana-kondoo na kumuchinja kwa sikukuu ya Pasaka. Mutatwaa majani ya hisopo na kuyachovya katika damu ndani ya beseni na kupakaa vizingiti na miimo yote miwili ya milango ya nyumba zenu. Mutu yeyote asitoke inje ya nyumba usiku ule mpaka asubui. Maana Yawe atapita kuwaua Wamisri. Lakini atakapoona damu iliyopakwa kwenye vizingiti na miimo ya nyumba zenu, atapita na wala hatamuruhusu mwangamizaji kuingia katika nyumba zenu na kuwaua. Mushike jambo hili ninyi na wazao wenu kama agizo la milele. Mutakapoingia katika inchi ile ambayo Yawe atawapa, kama alivyoahidi, munapaswa kulitimiza. Kila wakati watoto wenu watakapowauliza: ‘Jambo hili lina maana gani?’, ninyi mutawajibu: ‘Hii ni sadaka ya Pasaka kwa Yawe, kwa sababu alipita nyumba za Waisraeli katika inchi ya Misri. Aliwaua Wamisri, lakini sisi hakutuua.’ ” Waisraeli wakainamisha vichwa na kumwabudu Yawe. Kisha Waisraeli wakaenda, wakafanya kama vile walivyoambiwa na Musa na Haruni kulingana na amri ya Yawe. Katikati ya usiku, Yawe akawaua wazaliwa wa kwanza wote wa Misri. Wote walikufa, tangu muzaliwa wa kwanza wa mufalme wa Misri, murizi wa ufalme, mpaka muzaliwa wa kwanza wa mufungwa katika kifungo. Hata wazaliwa wa kwanza wa nyama nao walikufa. Basi mufalme, watumishi wake na wakaaji wote wa Misri wakaamuka usiku. Kukakuwa kilio kikubwa katika inchi yote ya Misri kwa maana hakukuwa hata nyumba moja ambamo mutu hakukufa. Halafu mufalme wa Misri akaita Musa na Haruni, usiku uleule, akawaambia: “Musimame! Muondoke kati ya watu wangu. Muende, ninyi pamoja na wale Waisraeli, mumutumikie Yawe kama vile mulivyosema. Mutwae makundi yenu ya kondoo na ngombe, muondoke. Muniombee na mimi baraka.” Wamisri wakawasukuma Waisraeli waondoke haraka, wakisema: “Hakika tutakufa sisi wote!” Basi, Waisraeli wakatwaa unga wao uliopondwa mbele haujatiwa chachu na mabakuli yao ya kupondea mikate walikuwa wamezifunga kwa nguo na kubeba juu ya mabega. Waisraeli walikuwa wamekwisha kufanya kama vile Musa alivyowaagiza pale mbele. Waliwaomba Wamisri wawapatie vyombo vya feza na zahabu na nguo. Naye Yawe alikwisha kuwafanya Waisraeli wapate kukubaliwa mbele ya Wamisri, nao Wamisri wakawapa kila kitu walichoomba. Ndivyo Waisraeli walivyonyanganya Wamisri mali yao. Waisraeli waliondoka katika muji wa Ramesesi, wakasafiri kwa miguu kuelekea Sukoti. Walikuwa wanaume yapata elfu mia sita, bila kuhesabu wanawake na watoto. Kulikuwa vilevile kundi la watu wengine waliokwenda pamoja nao na mifugo mingi, kondoo na ngombe. Kwa sababu walikuwa wameondoka Misri kwa haraka, hawakuweza kutayarisha chakula cha safari, ila tu ule unga uliopondwa bila kutiwa chachu. Basi, wakapika mikate isiyotiwa chachu. Waisraeli walikuwa wameishi katika inchi ya Misri kwa muda wa miaka mia ine na makumi tatu. Katika siku ya mwisho ya mwaka wa mia ine na makumi tatu, siku ileile ndipo makabila yote ya Yawe yaliondoka katika inchi ya Misri. Usiku ule ambao Yawe alikesha kwa kuwatoa Waisraeli katika inchi ya Misri, unapaswa kukumbukwa na Waisraeli wote na vizazi vyao vyote, kama usiku wa kukesha kwa heshima ya Yawe. Yawe akamwambia Musa na Haruni: “Haya ndiyo maagizo juu ya Pasaka. Mugeni yeyote hatashiriki chakula cha Pasaka. Lakini mutumwa yeyote aliyenunuliwa kwa feza, nyuma ya kumutahiri, ataruhusiwa kushiriki. Musafiri yeyote, wala mutumishi yeyote wa mushahara, hatashiriki chakula hicho. Mwana-kondoo wa Pasaka atakuliwa katika nyumba moja. Hamutatoa nyama yoyote inje ya nyumba alimochinjiwa, wala hamutavunja hata mufupa mumoja wa nyama wa Pasaka. Waisraeli wote pamoja watashika sikukuu hiyo. Mugeni yeyote anayeishi kati yenu akipenda kushiriki sikukuu ya Pasaka, anapaswa kwanza kutahiri wanaume wote wa nyumba yake. Halafu atahesabiwa kuwa kama mwenyeji na kuruhusiwa kushiriki. Mwanaume yeyote asiyetahiriwa asishiriki hata kidogo. Sheria zilezile zitaelekea Mwisraeli aliyezaliwa katika inchi na wageni watakaoishi kati yenu.” Waisraeli wote walitii sheria hiyo na kufanya kama vile Yawe alivyowaagiza Musa na Haruni. Siku hiyohiyo Yawe aliwatoa Waisraeli katika inchi ya Misri kwa makundi. Yawe alimwambia Musa: “Unitakasie wazaliwa wote wa kwanza, maana wazaliwa wote wa kwanza wa Waisraeli ni wangu, ikuwe wanaume au wanyama.” Musa akawaambia watu: “Mukumbuke siku hii muliyotoka inchi ya Misri ambako mulikuwa watumwa. Hii ndiyo siku Yawe alipowatoa humo kwa mukono wake wenye nguvu. Katika siku hii, musikule mukate uliotiwa chachu. Siku hii, mwezi wa kwanza wa Abibu, mutaondoka katika inchi ya Misri. Na wakati Yawe atakapowafikisha katika inchi ya Wakanana, Wahiti, Waamori, Wahivi, na Wayebusi, inchi ambayo aliwaapia babu zenu kwamba atawapa ninyi, inchi inayotiririka maziwa na asali, munapaswa kushika sikukuu hii kila mwaka katika mwezi huu wa kwanza. Kwa muda wa siku saba mutakula mikate isiyotiwa chachu, na katika siku ya saba mutafanya sikukuu kwa heshima ya Yawe. Kwa muda ule wa siku saba mutakula mikate isiyotiwa chachu. Kusikuwe mikate iliyotiwa chachu, wala chachu yoyote kati yenu na katika inchi yenu yote. Siku hiyo mutawaambia watoto wenu kwamba munafanya hivyo kwa sababu ya jambo Yawe alilowafanyia mulipoondoka katika inchi ya Misri. Na mambo haya yatakuwa ukumbusho, kama vile kitambulisho katika mikono yenu au katika paji la nyuso zenu; kusudi kiwakumbushe siku zote sheria ya Yawe. Maana, Yawe amewatoa katika inchi ya Misri kwa mukono wenye nguvu. Kwa hiyo, mutashika sikukuu hii kwa wakati uliopangwa, kila mwaka.” Musa akaendelea kuwaambia watu: “Vilevile, wakati Yawe atakapowafikisha katika inchi ya Wakanana na kuwapa inchi ile kama vile alivyowaapia ninyi na babu zenu, munapaswa kumuwekea Yawe kila muzaliwa wenu wa kwanza mwanaume. Kila muzaliwa wa kwanza dume wa mifugo yenu atakuwa wa Yawe. Lakini muzaliwa wa kwanza dume wa punda utamukomboa kwa kulipa mwana-kondoo; kama sivyo, utamwua kwa kumuvunja shingo. Kila muzaliwa wa kwanza wa kiume wa mwanadamu utamukomboa. Kama kisha mwana wako akiuliza maana ya jambo hili, utamwambia: ‘Kwa nguvu ya mukono wake, Yawe alitutoa katika inchi ya Misri ambako tulikuwa watumwa. Mufalme wa Misri kwa ugumu wake alikataa kutuachilia tuondoke. Kwa hiyo Yawe akamwua kila muzaliwa wa kwanza katika inchi ya Misri, muzaliwa wa kwanza wa mwanadamu na wa nyama. Basi, mimi ninamutolea Yawe sadaka kila muzaliwa wa kwanza dume wa mifugo yangu. Lakini kila muzaliwa wa kwanza wa wana wangu ninamukomboa.’ Jambo hili litakuwa kama kitambulisho katika mukono wako au utepe katika paji la uso wako, kwamba Yawe alitutoa katika inchi ya Misri kwa mukono wenye nguvu.” Wakati mufalme wa Misri alipowaachilia Waisraeli wajiendee, Mungu hakuwapitisha katika inchi ya Wafilistini, ingawa njia hiyo ilikuwa ya karibu. Mungu alisema: “Sipendi watu hawa wabadilishe nia na kurudi Misri wakijua kama itawapasa kupigana vita.” Pahali pake, Mungu akawapitisha Waisraeli katika njia ya muzunguko kupitia katika jangwa, kuelekea bahari Nyekundu. Waisraeli wakaondoka katika inchi ya Misri wakiwa wamejitayarisha kwa vita. Musa alipeleka mifupa ya Yosefu kama vile Yosefu alivyoagiza mbele ya kufa kwake. Alikuwa amewaapisha Waisraeli akisema: “Mungu atakapowafikia kuwatoa katika inchi hii, munapaswa kupeleka mifupa yangu kutoka hapa pamoja nanyi.” Basi, Waisraeli wakaondoka Sukoti, wakapiga kambi kule Etamu, kwenye ukingo wa jangwa. Muchana, Yawe aliwatangulia katika munara wa wingu kwa kuwaonyesha njia. Na usiku aliwatangulia katika munara wa moto kuwaangazia, kusudi waweze kusafiri muchana na usiku. Munara wa wingu wakati wa muchana na munara wa moto wakati wa usiku haikukosekana kuwatangulia Waisraeli. Kisha, Yawe akamwambia Musa: “Uwaambie Waisraeli warudi nyuma, wapige kambi mbele ya Pi-Hahiroti, kati ya muji wa Migdoli na bahari Nyekundu, mbele ya Bali-Sefoni. Mutapiga kambi mbele yake karibu na bahari. Maana, mufalme wa Misri atafikiri: ‘Hao Waisraeli wanatangatanga, nalo jangwa limewazuia wasiweze kutoka.’ Halafu mimi nitafanya moyo wa mufalme wa Misri kuwa mugumu, naye atawafuatilia. Nami nitajipatia utukufu kwa kumwangamiza yeye na jeshi lake. Halafu Wamisri watatambua kwamba mimi ni Yawe.” Basi, Waisraeli wakafanya hivyo. Mufalme wa Misri aliposikia kwamba Waisraeli wamekimbia, yeye na wakubwa wake walibadilisha mafikiri yao, wakasema: “Tumefanya nini kwa kuwaachilia Waisraeli waende zao wasitutumikie tena?” Basi, mufalme akatayarisha gari lake la vita na jeshi lake. Alitwaa magari yake bora ya vita mia sita na magari yote mengine ya kivita ya Misri yakiongozwa na wakubwa wa kijeshi. Yawe akafanya moyo wa mufalme wa Misri kuwa mugumu, naye akawafuatilia Waisraeli ambao walikuwa wameondoka Misri katika uhuru. Wamisri pamoja na farasi wao wote, magari ya vita na wapanda-farasi wake waliwafuata Waisraeli. Wakawakuta wamepiga kambi kando ya bahari, karibu na Pi-Hahiroti, mbele ya Bali-Sefoni. Waisraeli walipoinua macho na kumwona mufalme wa Misri akikuja na jeshi lake nyuma yao, wakashikwa na hofu kubwa, wakamulilia Yawe. Wakamwambia Musa: “Hakukuwa makaburi ya kutosha katika inchi ya Misri hata ukatuleta tukufie huku katika jangwa? Kwa nini umetufanya tutoke katika inchi ya Misri? Hatukukuambia mambo haya tulipokuwa bado Misri? Tulikuambia utuache tuendelee kuwatumikia Wamisri. Ingalikuwa vizuri kuwatumikia Wamisri kuliko kukufia huku katika jangwa.” Musa akawaambia Waisraeli: “Musiogope! Musimame imara! Leo mutaona jinsi Yawe atakavyowaokoa. Maana, hawa Wamisri munaowaona leo, hamutawaona tena. Yawe atawapigania. Ninyi mutakaa kimya tu.” Yawe akamwambia Musa: “Kwa nini munanililia? Uwaambie Waisraeli waendelee mbele. Inua fimbo yako na kuielekeza juu ya bahari. Maji yatagawanyika na Waisraeli wataweza kuvuka katikati ya bahari pahali pakavu. Mimi nitafanya mioyo ya Wamisri kuwa migumu, nao watawafuatilia katikati ya bahari. Nami nitajipatia utukufu kutokana na kuangamizwa kwa mufalme wa Misri na jeshi lake, magari yake ya vita pamoja na wapanda-farasi wake. Hakika, nitatukuzwa kwa kumwangamiza mufalme na jeshi lake, pamoja na magari yake na wapanda-farasi. Nao Wamisri watajua kwamba mimi ni Yawe.” Basi, malaika wa Mungu aliyekuwa mbele ya kundi la Waisraeli akaondoka akakaa nyuma yao. Na ule munara wa wingu vilevile ukaondoka mbele ukasimama nyuma yao. Ukakaa katikati ya Waisraeli na Wamisri. Lile wingu likawatia Wamisri giza, lakini likawaangazia Waisraeli usiku. Kwa hiyo, makundi hayo mawili, jeshi la mufalme wa Misri na kundi la Waisraeli, hayakukaribiana usiku kucha. Musa akanyoosha mukono wake juu ya bahari, naye Yawe akasukuma bahari nyuma kwa upepo mukali toka upande wa mashariki. Upepo ule ulivuma usiku kucha, ukagawanya bahari sehemu mbili na katikati kukatokea inchi kavu. Waisraeli wakapita katikati ya bahari pahali pakavu, kuta za maji zikiwa upande wao wa kuume na wa kushoto. Wamisri wakawafuata kwa kupitia inchi kavu iliyokuwa katikati ya bahari pamoja na farasi wao, magari yao ya vita na wapanda-farasi wao wote. Karibu na mapambazuko, Yawe akaangalia jeshi la Wamisri kutoka katika ule munara wa moto na ule munara wa wingu, akalitia hofu kubwa. Alikwamisha magurudumu ya magari yao, yakakuwa yakienda kwa shida sana. Halafu Wamisri wakasema: “Tuwakimbie Waisraeli! Yawe anawapigania Waisraeli mbele yetu.” Kisha Yawe akamwambia Musa: “Nyoosha mukono wako juu ya bahari, kusudi maji yarudie na kuwafunika Wamisri pamoja na magari yao na wapanda-farasi wao.” Basi, Musa akanyoosha mukono wake juu ya bahari na kulipopambazuka bahari ikarudilia hali yake ilivyokuwa. Wamisri wakajaribu kukimbia maji lakini Yawe akawasukumizia ndani ya bahari. Maji yakafunika magari pamoja na wapanda-farasi. Jeshi lote la mufalme wa Misri lililokuwa limewafuatilia Waisraeli likakufa katika bahari. Hakukuponyoka Mumisri hata mumoja. Lakini Waisraeli walipita katikati ya bahari pahali pakavu, kuta za maji zikiwa zimesimama upande wao wa kuume na wa kushoto. Siku hiyo Yawe akawaokoa Waisraeli toka mikono ya Wamisri. Waisraeli wakawaona maiti ya Wamisri pembeni ya bahari. Waisraeli walipoona tendo hilo la ajabu Yawe alilofanya mbele ya Wamisri, wakamwogopa. Wakamwamini Yawe na Musa mutumishi wake. Kisha, Musa pamoja na Waisraeli wakamwimbia Yawe wimbo huu: “Nitamwimbia Yawe, maana ameshinda kwa utukufu; farasi na mupanda-farasi wake amewatupa katika bahari. Yawe ananijalia nguvu na uwezo, yeye mwenyewe ndiye anayeniokoa. Yeye ni Mungu wangu nami nitamusifu; ni Mungu wa baba yangu nami nitamutukuza. Yawe ni shujaa kwa vita; Yawe ndilo jina lake. “Magari na majeshi ya mufalme wa Misri ameyatumbukiza ndani ya bahari; majemadari wake wachaguliwa wamezama katika bahari Nyekundu. Vilindi vya maji vimewafunika, wameporomoka katika bahari kama jiwe. “Mukono wako wa kuume, ee Yawe, unatukuka kwa nguvu; kwa mukono wako wa kuume, ee Yawe, unawaponda waadui. Kwa wingi wa ukubwa wako unawaangamiza wapinzani wako; unawapulizia kasirani yako nayo inawateketeza kama maganda. Kwa pumzi ya pua yako maji yalilundikana, mawimbi yakasimama wima kama ukuta; vilindi katikati ya bahari vikagandamana. Adui akajisemesha: ‘Nitawafuata na kuwakamata; nitagawanya vitu mpaka hamu yangu iishe. Tutafuta upanga wetu, tutawaangamiza kwa mukono wetu.’ Lakini wewe uliuvumisha upepo wako, nayo bahari ikawafunika. Walizama ndani ya maji kama risasi. “Ewe Yawe, ni nani kati ya miungu anayelingana nawe? Ni nani aliyekuwa kama wewe unayekuwa mutakatifu mukubwa, unayetisha kwa matendo matukufu, unayetenda mambo ya ajabu? Ulinyoosha mukono wako wa kuume, nayo inchi ikawameza waadui zetu. “Kwa wema wako mukubwa umewaongoza watu uliowakomboa, kwa nguvu yako umewaongoza kwenye makao yako matakatifu. Watu wa mataifa wamesikia hayo wakatetemeka; Wafilistini wamepatwa na kitisho. Wakubwa wa Edomu wamefazaishwa; viongozi wa Moabu wamepatwa na woga mukubwa; wakaaji wote wa Kanana wamevunjika moyo. Kitisho na hofu vimewashika. Kwa sababu ya ukubwa wa nguvu zako, wao wamenyamaza kimya kama jiwe, mpaka watu wako, ee Yawe, wapite, mpaka watu wale uliowakomboa wamewapita. Wewe utawaleta watu wako na kuwapanda juu ya mulima wako, pale ulipochagua, ee Yawe, kuwa makao yako, pahali patakatifu, ee Yawe, ulipojenga kwa mikono yako. “Wewe, ee Yawe, unatawala milele na milele.” Wakati farasi wa mufalme wa Misri na magari yake pamoja na wapanda-farasi wake walipoingia pahali pakavu katika bahari, Yawe aliyarudisha maji ya bahari yakawafunika. Lakini Waisraeli waliendelea kutembea pakavu katikati ya bahari. Basi nabii Miriamu, dada ya Haruni, akatwaa ngoma katika mukono, na wanawake wengine wote wakamufuata wakiwa na ngoma zao ndogo wakicheza. Miriamu akawaongoza kwa kuimba: “Mumwimbie Yawe maana ameshinda kwa utukufu. Farasi na mupanda-farasi wake amewatupa ndani ya bahari.” Kisha, Musa akawaongoza Waisraeli kutoka bahari Nyekundu, wakaenda mpaka kwenye jangwa la Suri. Wakasafiri kwa muda wa siku tatu katika jangwa bila kuona maji yoyote. Walipofika pahali panapoitwa Mara, hawakuweza kunywa maji ya Mara kwa sababu yalikuwa machungu. Kwa sababu hiyo pahali pale pakaitwa Mara, ni kusema “Uchungu”. Basi, watu wote wakamunungunikia Musa wakisema: “Sasa tutakunywa nini?” Halafu Musa akamulilia Yawe, naye akamwonyesha kipande cha muti, na Musa akakitumbukiza katika maji. Maji hayo yakakuwa mazuri. Kule Mungu aliwapa Waisraeli sharti na agizo, kusudi awapime, akawaambia: “Ikiwa mutaisikiliza kwa uaminifu sauti yangu mimi Yawe, Mungu wenu, kutenda yale yanayokuwa sawa mbele yangu, na kuheshimu amri na masharti yangu yote, basi, mimi sitawaletea yale magonjwa niliyowaletea Wamisri. Kwa sababu, mimi ni Yawe ninayewaponya ninyi.” Kisha Waisraeli wakafika kule Elimu ambako kulikuwa chemichemi kumi na mbili na mingazi makumi saba. Wakapiga kambi yao kule karibu na maji. Waisraeli wote wakasafiri toka Elimu na kufika katika jangwa la Sini kati ya Elimu na Sinai. Hii ilikuwa siku ya kumi na tano ya mwezi wa pili tangu walipoondoka inchi ya Misri. Basi, Waisraeli wote pamoja wakamunungunikia Musa na Haruni kule katika jangwa. Wakasema hivi: “Heri Yawe angelituua tulipokuwa katika inchi ya Misri ambako tulikaa, tukakula nyama na mikate hata tukashiba. Lakini ninyi mumetuleta huku katika jangwa kwa kuua jamii hii yote kwa njaa!” Halafu Yawe akamwambia Musa: “Mimi nitawanyeshea mikate kutoka mbinguni. Kila siku watu watatoka na kukusanya chakula cha siku hiyo. Kwa njia hii nitawapima nione kama watafuata sheria zangu au hawatazifuata. Lakini siku ya sita, wakati watakapotayarisha chakula walichokusanya, kipimo kile kitakuwa mara mbili ya chakula cha kila siku.” Basi, Musa na Haruni wakawaambia watu wote wa Israeli: “Magaribi, mutatambua kwamba Yawe ndiye aliyewatoa katika inchi ya Misri! Tena, kesho asubui mutaona utukufu wa Yawe maana ameyasikia manunguniko muliyomunungunikia. Sisi ni nani hata mutunungunikie?” Tena Musa akasema: “Magaribi, Yawe atawapa nyama mupate kula na asubui atawapa mikate mupate kula na kushiba. Maana yeye ameyasikia manunguniko muliyomunungunikia. Sisi ni nani hata mutunungunikie? Musitunungunikie sisi lakini mumunungunikie Yawe.” Kisha Musa akamwambia Haruni: “Uwaambie Waisraeli wote wakusanyike mbele ya Yawe, maana ameyasikia manunguniko yao.” Wakati Haruni alipokuwa akizungumuza na Waisraeli wote pamoja, watu wote wakaangalia kule katika jangwa na mara moja utukufu wa Yawe ukaonekana katika mawingu. Yawe akamwambia Musa: “Nimesikia manunguniko ya Waisraeli. Basi, uwaambie kwamba wakati wa magaribi watakula nyama na asubui watakula mukate. Hapo ndipo mutakapotambua kwamba mimi ni Yawe, Mungu wenu.” Basi, kwa wakati wa magaribi kukakuja kwale wengi, wakafunika kambi ya Waisraeli. Asubui yake kukatokea umande, ukatanda kandokando ya kambi yao. Umande ule ulipotoweka, kukabaki kule katika jangwa kitu kama mukate mwembamba na mwepesi. Waisraeli walipoona kitu kile wakashangaa, wakaulizana: “Nini hii?” Hawakujua kilikuwa kitu gani. Basi, Musa akawaambia: “Huu ni mukate ambao Yawe amewapa mukule. Yawe ameamuru mufanye hivi: kila mutu akusanye chakula kipimo anachoweza kula. Ataokota kipimo cha litre ine kwa kila mutu katika hema yake.” Basi, Waisraeli wakafanya hivyo na ikakuwa kwamba wengine waliokota kwa wingi na wengine kidogo. Lakini wote walipopima kiasi walichookota katika kipimo cha litre ine, walitambua kwamba aliyeokota kingi hakukuwa na cha zaidi na aliyeokota kidogo, hakupungukiwa. Kila mumoja alikuwa ameokota kiasi alichoweza kula. Musa akawaambia watu: “Mutu yeyote asiache chakula hicho mpaka asubui.” Lakini watu hawakumusikiliza Musa. Wamoja kati yao walijiwekea chakula mpaka asubui. Lakini asubui chakula hicho kikakuwa kimeoza na kuwa na vidudu. Musa akawakasirikia sana watu. Basi, kila asubui walikusanya chakula kila mutu kipimo alichohitaji kula. Jua lilipopanda juu na kuwa kali, kile chakula kingine kiliyeyuka. Katika siku ya sita, Waisraeli walikusanya chakula hicho mara mbili, vipimo viwili vya litre ine kwa kila mutu. Basi, wazee wote wa Waisraeli wakamwendea Musa, wakamwelezea jambo hilo. Musa akawaambia: “Hii ndiyo amri ya Yawe. Kesho ni siku ya mapumziko. Ni Sabato takatifu ya Yawe. Basi, muende mupike au kuchemusha kile chakula munachohitaji leo na chakula kitakachobakia mukiweke mpaka kesho.” Basi, wakafanya hivyo na kuacha chakula kingine mpaka kesho yake kama vile Musa alivyosema. Asubui yake waliona kwamba hakikuharibika wala kuwa na vidudu. Basi, Musa akawaambia: “Mukule chakula hicho kilichobakia kwa sababu leo ni Sabato ya Yawe. Leo hamutapata chakula kule inje. Kwa siku sita mutakuwa mukikusanya chakula hiki, lakini siku ya saba ambayo ni Sabato hakitakuwa.” Kwa siku ya saba watu wamoja walitoka kwenda kutafuta chakula, lakini hawakukipata. Hapo Yawe akamwambia Musa: “Mpaka wakati gani mutakataa kutii amri na sheria zangu? Mufahamu kwamba mimi Yawe nimewapa siku ya Sabato, ndiyo maana nimewapa chakula cha siku mbili kwa siku ya sita. Basi, kila mutu apumzike ndani ya nyumba yake. Mutu yeyote asitoke katika siku ya saba.” Kwa hiyo, watu walipumzika siku ya saba. Waisraeli wakaita chakula hicho “Mana.” Kilikuwa kama mbegu za mutama mweupe na onjo yake ilikuwa kama mukate mwembamba uliotiwa asali. Musa akawaambia: “Hili ndilo agizo la Yawe: Mutwae kipimo kimoja cha litre ine ya mana na kukiweka kwa ajili ya wazao wenu, kusudi waweze kuona chakula nilichowakulisha katika jangwa wakati nilipowatoa katika inchi ya Misri.” Musa akamwambia Haruni: “Twaa kopo, utie ndani yake kipimo kimoja cha litre ine ya mana na kuiweka mbele ya Yawe, ikuwe kwa ajili ya wazao wenu.” Basi, Haruni aliweka mana Pahali Patakatifu mbele ya Sunduku la Agano kusudi ilindwe kama vile Yawe alivyomwagiza Musa. Waisraeli walikula mana kwa muda wa miaka makumi ine, mpaka walipofika katika inchi iliyofaa kwa kuishi, ni kusema mpaka walipovuka mupaka wa Kanana. (Posho ya mana ilikuwa sehemu ya kumi ya kipimo cha kawaida kinachoitwa efa.) Kutoka jangwa la Sini, Waisraeli wote pamoja wakasafiri hatua kwa hatua kama vile Yawe alivyoamuru. Watu wakapiga kambi kule Refidimu. Lakini kule hakukukuwa maji ya kunywa. Kwa hiyo watu wakamunungunikia Musa wakisema: “Utupatie maji ya kunywa.” Musa akawauliza: “Mbona munaninungunikia? Mbona munamujaribu Yawe?” Lakini wote walikuwa na kiu, wakamunungunikia Musa wakisema: “Kwa nini ulitutoa kule Misri utuue kwa kiu, sisi wote na watoto wetu na mifugo yetu?” Basi, Musa akamulilia Yawe akisema: “Nitawafanyia nini watu hawa? Wako karibu kunipiga mawe!” Yawe akamwambia Musa: “Pita mbele ya watu hawa ukipeleka wazee wao wamoja. Twaa vilevile katika mukono wako ile fimbo uliyoipiga nayo muto Nili. Angalia mimi nitasimama mbele yako juu ya jiwe la mulima wa Horebu, nawe utapiga lile jiwe na maji yatabubujika kutoka mule kusudi watu wote wapate kunywa.” Basi, Musa akafanya hivyo mbele ya wazee wa Waisraeli. Pahali pale Musa akapaita “Masa” na “Meriba”, ni kusema “Ujaribu” na “Magombano”, kwa sababu Waisraeli walimugombanisha na kumujaribu Yawe wakisema: “Kweli Yawe yuko pamoja nasi?” Waamaleki walikuja na kupigana na Waisraeli kule Refidimu. Musa akamwambia Yoshua: “Chagua wanaume uende upigane na Waamaleki. Kesho nitasimama juu ya kilele cha kilima, nikishika katika mukono wangu ile fimbo ya Mungu.” Basi, Yoshua akafanya kama vile Musa alivyosema, akaenda kupigana na Waamaleki. Musa, Haruni na Huri wakapanda juu ya kilele cha kilima. Ikakuwa wakati wote Musa alipoinua mukono wake juu, Waisraeli walishinda na alipouteremusha, Waamaleki walishinda. Lakini kisha muda, mikono ya Musa ikachoka. Kwa hiyo Haruni na Huri wakatwaa jiwe wakaliweka karibu na Musa naye akaikaa. Kisha wakaishika na kuiinua mikono yake. Mumoja akauinua mukono wa kuume na mwingine mukono wa kushoto. Hivyo mikono ya Musa ikabaki imara ikiwa imeinuliwa juu mpaka jua lilipotua. Yoshua akawakatakata Waamaleki. Kisha Yawe akamwambia Musa: “Uandike jambo hili katika kitabu, likuwe ukumbusho. Tena umwambie Yoshua kwamba nitawafuta kabisa Waamaleki katika dunia.” Musa akajenga mazabahu na kuita mazabahu hiyo “Yawe ni Bendera Yangu”, akisema: “Muinue juu bendera ya Yawe! Yawe atapigana na Waamaleki kizazi kwa kizazi!” Yetro, kuhani wa Midiani, baba mukwe wa Musa, alisikia juu ya mambo yote ambayo Yawe alimutendea Musa na Waisraeli alipowatoa katika inchi ya Misri. Kwa hiyo Yetro, akiwa na Sipora muke wa Musa ambaye Musa alikuwa amemurudisha kwa baba yake, alimwendea Musa, pamoja na watoto wawili wa Musa. Mutoto wa kwanza aliitwa Gersomi. Musa alimupa jina hili kwa vile alisema: “Nimekimbilia katika inchi ya kigeni.” Wa pili aliitwa Eliezeri, kwa vile Musa alisema: “Mungu wa baba yangu ndiye aliyenisaidia nisiuawe na mufalme wa Misri.” Yetro, baba mukwe wa Musa, alikuja pamoja na binti yake, ni kusema muke wa Musa, pamoja na watoto. Akamukuta Musa katika jangwa alikokuwa amepiga kambi kwenye mulima wa Mungu. Musa alipoambiwa kwamba baba mukwe wake pamoja na muke wake na wana wake wawili wanakuja, akatoka kwenda kumupokea baba mukwe wake, akiinama mbele yake na kumubusu. Wakasalimiana, kisha wakaingia ndani ya hema. Musa akamwelezea baba mukwe wake mambo yote Yawe aliyomutendea mufalme wa Misri na Wamisri kwa ajili ya Waisraeli. Akamwambia vilevile juu ya shida zote zilizowapata katika safari na jinsi Yawe alivyowaokoa. Yetro akafurahishwa na yote Yawe aliyotenda kwa ajili ya Waisraeli, kwa kuwaokoa toka katika mikono ya Wamisri. Yetro akasema: “Atukuzwe Yawe ambaye amewaokoa toka katika mikono ya Wamisri na kutoka katika mukono wa mufalme wa Misri. Sasa ninajua kwamba Yawe ni mukubwa kuliko miungu yote, maana amewakomboa watu hawa toka katika mikono ya Wamisri ambao waliwatendea ubaya.” Halafu Yetro, baba mukwe wa Musa, akamutolea Mungu sadaka za kuteketezwa kwa moto na sadaka zingine. Naye Haruni akakuja pamoja na wazee wa Israeli kwa kula chakula pamoja na Yetro, mbele ya Yawe. Kesho yake, Musa akaikaa kwa kuamua matatizo ya Waisraeli, nao wakasimama wakiwa wamemuzunguka, tangu asubui mpaka magaribi. Yetro, baba mukwe wa Musa, alipoona mambo yote ambayo Musa aliwafanyia Waisraeli, akamwuliza: “Kwa nini unawafanyia watu mambo haya? Mbona unaikaa peke yako wakati watu wamekuzunguka tangu asubui mpaka magaribi?” Musa akamujibu baba mukwe wake: “Kwa sababu watu wanakuja kwangu kuuliza mapenzi ya Mungu. Wakiwa na ugomvi wowote wao wanakuja kwangu nami ninaamua kati ya mutu na mwenzake na kuwafundisha masharti ya Mungu na maamuzi yake.” Basi, Yetro akamwambia Musa: “Unavyofanya si vizuri! Utajichokesha mwenyewe na hawa watu, maana hii ni kazi ngumu usiyoweza kuifanya peke yako. Sikiliza shauri langu kwako na Mungu akuwe pamoja nawe. Wewe utawasimamia watu mbele ya Mungu na kumuletea Mungu matatizo yao. Vilevile utawafundisha masharti na sheria ya Mungu na kuwaonyesha jinsi inavyowapasa kuishi na kufanya. Lakini juu ya mambo mengine, chagua kati ya watu wote, watu wanaostahili, watu wanaomwogopa Mungu, waaminifu na wanaochukia kituliro. Uwape hao mamlaka, wakuwe na kazi ya kuwasimamia watu katika makundi ya watu elfu, mia, makumi tano na kumikumi. Hao ndio watakaokuwa na vikao kila siku kutatua matatizo ya watu. Matatizo magumu watakuletea wewe, lakini yale madogomadogo watayaamua wenyewe. Kwa njia hiyo utaweza kufanya kazi yako kuwa nyepesi kwa vile watashirikiana nawe katika kazi hiyo. Ukifanya hivyo na kama ndivyo Mungu anavyotaka, utaweza kuvumilia na watu hawa wote wataweza kurudi kwao kwa amani.” Musa akasikiliza shauri lile la baba mukwe wake na kufanya kama vile alivyoshauriwa. Basi, akachagua watu wenye uwezo kati ya Waisraeli, akawafanya kuwa viongozi wa makundi ya watu elfu, watu mia, watu makumi tano na watu kumikumi. Nao wakakuwa wanaamua matatizo ya watu kila wakati. Matatizo magumu walimuletea Musa, lakini yale madogomadogo waliyatatua wao wenyewe. Kisha kufanya hivyo, Musa na baba mukwe wake wakaagana, naye Yetro akarudi katika inchi yake. Siku ya kwanza ya mwezi wa tatu tangu walipotoka katika inchi ya Misri, watu wa Israeli wakafika katika jangwa la Sinai. Walipoondoka Refidimu na kufika jangwa la Sinai, kule wakapiga kambi mbele ya mulima Sinai. Basi, Musa akapanda juu kwenye mulima kwa Mungu. Halafu Yawe akamwita Musa kutoka kule juu ya mulima, akamwambia: “Hivi ndivyo utakavyowaambia wazao wa Yakobo, wale Waisraeli: ‘Ninyi wenyewe mumeona jinsi nilivyowatendea Wamisri na jinsi nilivyowapeleka ninyi kama vile tai anavyopeleka watoto wake kwa mabawa, nikawaleta kwangu. Sasa basi, kama mukitii sauti yangu na kushika agano langu, mutakuwa watu wangu wachaguliwa kati ya mataifa yote, maana dunia yote ni yangu. Mutakuwa kwangu ufalme wa makuhani na taifa takatifu.’ Hayo ndiyo maneno utakayowaambia Waisraeli.” Basi, Musa akarudi, akawakusanya pamoja wazee wa Waisraeli na kuwaambia maneno hayo aliyoamuriwa na Yawe. Watu wote wakaitikia kwa pamoja wakisema: “Mambo yote Yawe aliyosema, tutayafanya.” Musa akamujulisha Yawe jibu lile la watu. Yawe akamwambia Musa: “Basi, mimi nitakufikia katika wingu zito kusudi Waisraeli wapate kunisikia ninaposema nawe na kukuamini siku zote.” Kisha Musa akamwambia Mungu jinsi watu walivyosema. Yawe akamwambia Musa: “Kwenda kwa watu uwatakase leo na kesho. Uwaambie wafue nguo zao wakuwe tayari kwa kesho kutwa, maana siku hiyo ya tatu mimi Yawe nitashuka juu ya mulima Sinai mbele ya watu wote. Tena wewe utawawekea watu mupaka kuzunguka mulima kuwaambia wajilinde sana wasipande juu kwenye mulima wala kugusa mupaka wake. Yeyote atakayegusa mulima, atauawa. Mutu asimuguse mutu yule. Atauawa kwa kupigwa mawe au mushale. Akuwe ni mutu au ni nyama, hataishi. Wakati baragumu itakapopigwa mufululizo, watu wote watakaribia mulima.” Basi, Musa akashuka toka juu ya mulima na kuwaendea watu, akawatakasa, nao wakafua nguo zao. Kisha akawaambia watu wote: “Kesho kutwa mukuwe tayari na mwanaume yeyote asimukaribie mwanamuke.” Basi, siku ya tatu asubui, kukatokea ngurumo na umeme na wingu zito juu ya mulima. Kukasikilika vilevile sauti kubwa ya baragumu ambayo iliwatetemesha watu wote katika kambi. Kisha Musa akawaongoza watu wote kutoka katika kambi, wakaenda kukutana na Mungu. Wote walikwenda wakajipanga chini ya mulima. Mulima wa Sinai ulikuwa umefunikwa na moshi kwa sababu Yawe alishuka juu yake katika moto. Moshi wa moto ule ulipanda juu kama moshi wa furu kubwa na mulima wote ukatetemeka kwa nguvu. Sauti ya baragumu ikazidi kuongezeka na Musa akaongea na Mungu. Mungu naye akamujibu katika ngurumo. Yawe akashuka juu ya mulima Sinai, akamwita Musa kutoka kule juu, naye Musa akapanda juu ya mulima. Kisha Yawe akamwambia Musa: “Shuka chini uwaonye watu wote wasikuje kuniona. Kama sivyo wengi wao wataangamia. Hata makuhani ambao wananikaribia wanapaswa kujitakasa, kama sivyo nitawaazibu.” Musa akamwambia Yawe: “Watu hawa hawawezi kupanda juu ya mulima wa Sinai maana wewe mwenyewe ulituamuru tuweke mupaka kuzunguka mulima na kuutakasa.” Yawe akasema: “Teremuka chini kisha urudi pamoja na Haruni. Lakini usiwaruhusu makuhani na watu wengine wapite mupaka na kuja kwangu, kama sivyo nitawaazibu.” Basi, Musa akashuka na kuwaambia Waisraeli mambo yote aliyoagizwa. Mungu alisema maneno haya yote: Mimi ni Yawe, Mungu wako, niliyekutoa katika inchi ya Misri, ambako ulikuwa mutumwa. Usikuwe na miungu mingine isipokuwa mimi. Usijifanyie sanamu ya miungu, wala mufano wa kitu chochote kinachokuwa juu mbinguni, wala kinachokuwa chini katika dunia, wala kinachokuwa ndani ya maji chini ya dunia. Usiiname mbele yao wala kuvitumikia, kwa sababu mimi Yawe, Mungu wako, ni Mungu mwenye wivu. Ninawaazibu wana kwa ajili ya maovu ya baba zao, hata kizazi cha tatu na cha ine cha wale wanaonichukia. Lakini ninawatendea mema maelfu ya wale wanaonipenda na kushika amri zangu. Usitaje bure jina langu mimi Yawe, Mungu wako, maana mimi Yawe sitaacha kumwazibu yeyote anayetaja bure jina langu. Usisahau kuiweka takatifu siku ya Sabato. Siku sita fanya kazi na tenda mambo yako yote. Lakini siku ya saba ni Sabato ya Yawe, Mungu wako. Siku hiyo usifanye kazi yoyote, wewe, wala mwana wako, wala binti yako, wala mutumwa wako, wala mujakazi wako, wala nyama wako wa kufugwa, wala mugeni anayekuwa katika nyumba yako. Maana kwa siku sita mimi Yawe niliumba mbingu na inchi, bahari na vyote vinavyokuwa ndani yake, kisha nikapumzika siku ya saba. Kwa hiyo mimi Yawe nilibariki siku ya Sabato, nikaitakasa. Uwaheshimu baba yako na mama yako, kusudi uishi maisha marefu katika inchi ninayokupatia mimi Yawe, Mungu wako. Usiue. Usizini. Usiibe. Usimushuhudie mwenzako uongo. Usitamani nyumba ya mwenzako, wala muke wake, wala mutumwa wake au mujakazi wake, wala ngombe wake, wala punda wake, wala kitu chochote mwenzako anachokuwa nacho. Watu waliposikia ngurumo na kuona umeme ukiwaka na kusikia sauti ya baragumu juu ya mulima uliokuwa unafuka moshi, wote wakaogopa na kutetemeka. Wote wakasimama mbali, wakamwambia Musa: Sema nasi wewe mwenyewe, nasi tutakusikiliza. Lakini Yawe asiseme nasi, tusikufe. Musa akawaambia: Musiogope, maana Mungu amekuja kuwapima kusudi mupate kumwogopa siku zote na musitende zambi. Watu wote wakasimama mbali wakati Musa alipokaribia lile wingu zito Mungu alimokuwa. Yawe akamwambia Musa: Uwaambie Waisraeli: Mumejionea ninyi wenyewe kwamba nimeongea nanyi kutoka mbinguni. Mutaniheshimu mimi peke yangu wala musijifanyie miungu ya feza wala ya zahabu. Ninyi mutanijengea mazabahu ya udongo. Juu yake mutanitolea kondoo wenu na ngombe wenu kama sadaka za kuteketezwa kwa moto na sadaka za amani. Pahali popote nitakapowakumbusha watu jina langu, pale pale mimi mwenyewe nitawafikia na kuwabariki. Kama mukinijengea mazabahu ya mawe, musiitengeneze kwa mawe ya kuchonga, maana mukitumia vyombo vya kuchonga mawe, mutaichafua. Wala musitengeneze mazabahu yenye ngazi za kupandia, mutu asipate kuona uchi wa yule anayepanda juu yake. Haya ndiyo maagizo utakayowapa Waisraeli: Ukimununua mutumwa Mwebrania, atakutumikia kwa miaka sita, lakini mwaka wa saba atakuwa huru na kuondoka, bila malipo. Kama alinunuliwa mbele hajaoa, ataondoka peke yake. Lakini kama alikuja na muke wake, basi, ataondoka na muke wake. Kama bwana wake alimwoea muke, akamuzalia watoto wanawake au wanaume, basi, yule mwanamuke na watoto wake watakuwa mali ya yule bwana wake na yule mutumwa ataondoka peke yake. Lakini kama mutumwa yule akisema kwamba anamupenda bwana wake, muke wake na watoto wake na hataki kuondoka na kuwa huru, basi, bwana wake atamuleta mbele ya Mungu. Kisha atamupeleka kwenye mulango au kwenye kizingiti na kumutoboa sikio lake kwa chuma chenye kuchongwa. Naye atamutumikia bwana wake maisha yake yote. Mutu akimwuzisha binti yake kuwa mujakazi, yule hatapata uhuru wake kama watumwa wanaume. Ikiwa yule bwana wake alimununua akuwe mumoja wa wake zake, kisha asipendezwe naye, yule bwana ataacha baba ya yule mujakazi amukomboe. Yule bwana hana haki ya kumwuzisha kwa watu wa mataifa mengine, akiwa amemudanganya. Kama ataamua kumwoesha kwa mwana wake, atamutendea mujakazi yule kama vile binti yake. Kama yule bwana akioa muke mwingine, anapaswa kuendelea kumutosheleza muke wake wa kwanza kwa chakula, nguo na haki zake za ndoa. Ikiwa yule bwana hatamutimizia haki hizo tatu, basi, muke ataondoka na kuwa huru bila malipo yoyote. Anayepiga mutu na kumwua, hakika anapaswa kuuawa. Lakini kama hakukuwa amemuvizia, lakini ni kwa musiba, basi, yule mwuaji ataweza kukimbilia usalama pahali nitakapowachagulia. Lakini mutu akimushambulia mwenzake kwa makusudi na kumwua kwa werevu, hata kama akikimbilia kwenye mazabahu, mutamutoa kule kwenye mazabahu yangu na kumwua. Anayemupiga baba yake au mama yake hakika atauawa. Anayemukamata mutu kwa kinguvu kusudi amwuzishe au kumufanya mutumwa wake, hakika atauawa. Anayemulaani baba yake au mama yake hakika atauawa. Watu wawili wakigombana, kisha mumoja akamupiga mwenzake jiwe au ngumi bila kumwua, lakini akigonjwa na kubaki katika kitanda, ikiwa yule aliyepigwa akisimama tena na kuweza kutembea kwa kutegemea fimbo, yule aliyemupiga atasamehewa. Lakini, atamulipa kwa ajili ya muda alioupoteza katika kitanda na kumutunza mpaka apone kabisa. Mutu akimupiga mutumwa wake au mujakazi wake kwa fimbo na kumwua palepale, hakika ataazibiwa. Lakini mutumwa yule au mujakazi yule akibaki muzima siku moja au mbili, bwana wake hataazibiwa, maana yule alikuwa ni mali yake. Wanaume wakipigana na kumwumiza mwanamuke mwenye mimba, hata mimba yake ikaharibika bila hasara ingine zaidi, yule aliyemwumiza atalipa feza kadiri mume wa mwanamuke yule atakavyodai na kama vile waamuzi watakavyoamua. Lakini kama kutakuwa hasara nyingine, basi, unapaswa kulipa uzima kwa uzima, jicho kwa jicho, jino kwa jino, mukono kwa mukono, muguu kwa muguu, kuchomwa moto kwa kuchomwa moto, kidonda kwa kidonda, na pigo kwa pigo. Mutu akimupiga mutumwa au mujakazi wake na kuliharibu jicho lake, anapaswa kumwachilia aende huru bila malipo kwa ajili ya jicho lake. Vilevile, akimupiga hata kumwongoa mutumwa wake au mujakazi wake jino, anapaswa kumwachilia huru kwa ajili ya jino lake. Ngombe akimupiga mutu pembe na kumwua, ngombe yule atauawa kwa kupigwa mawe na nyama yake haitakuliwa. Mwenye ngombe yule hatahukumiwa. Lakini kama ngombe yule amezoea kupiga watu pembe, na mwenye ngombe akaonywa lakini hakumufunga, kama ngombe yule akiua mume au muke, ngombe yule atapigwa mawe, na mwenye ngombe vilevile atauawa. Hata hivyo, yule mutu akilipishwa feza kwa kuokoa maisha yake, anapaswa kulipa kiasi kamili atakacholipishwa. Ngombe akimupiga mutoto wa mutu mwingine kwa pembe, shauri hili litaamuliwa kwa njia hiyohiyo. Kama ngombe yule akimupiga pembe mutumwa au mujakazi, mwenye ngombe atamulipa bwana wa yule mutumwa feza zenye bei ya shekeli makumi tatu na yule ngombe anapaswa kuuawa kwa kupigwa mawe. Mutu akiacha shimo wazi, au akichimba shimo kisha asilifunike, halafu ngombe au punda akatumbukia ndani, yule mwenye shimo lile anapaswa kulipa. Atatoa feza kwa mwenye nyama yule na nyama aliyekufa atakuwa wake. Ngombe wa mutu akimwumiza ngombe wa mutu mwingine na kumwua, basi, watu watamwuzisha yule ngombe aliyebaki muzima na kugawayana bei yake. Vilevile watagawayana yule ngombe aliyekufa. Lakini kama yule ngombe alikuwa amezoea kupiga wengine pembe na mwenye ngombe yule hakumufunga, yeye atalipa ngombe kwa ngombe na yule ngombe aliyeuawa atakuwa wake. Mutu akiiba ngombe au kondoo na kumuchinja au kumwuzisha, atalipa ngombe watano kwa kila ngombe na kondoo wane kwa kila kondoo. Mwizi akikamatwa yuko anavunja nyumba, naye akipigwa na kufa, aliyemwua hana kosa la mauaji. Lakini mwizi akishikwa wakati jua limechomoza na kuuawa, aliyemwua atakuwa na kosa. Mwizi anapaswa kulipa. Ikiwa hana kitu cha kulipa, basi, yeye mwenyewe atauzishwa kwa kulipa kile alichoiba. Kama nyama aliyeibwa, akuwe ni ngombe, punda au kondoo, akipatikana muzima kwa mwizi, basi, yule mwizi atalipa nyama wawili. Mutu akiwakulishia nyama wake katika shamba la mizabibu au kumwachilia nyama wake kula katika shamba la mutu mwingine, atalipa hasara ile kwa mazao bora ya shamba lake mwenyewe au shamba lake la mizabibu. Mutu akiwasha moto nao ukichoma miti ya miiba na kusambaa mpaka kuteketeza miganda ya ngano au ngano ya mutu mwingine ambayo bado haijavunwa au shamba lote likiteketea, aliyewasha moto ule anapaswa kulipa hasara ile yote. Mutu akimwachia mwenzake feza au mali nyingine amutunzie, kisha ikaibiwa ndani ya nyumba yake, mwizi akipatikana anapaswa kulipa bei yake mara mbili. Lakini mwizi asipopatikana, mwenye nyumba atakaribia mbele ya Mungu kwa kuhakikisha kwamba yeye hakuiba mali ya mwenzake. Kukitokea ubishi juu ya ngombe, au punda, au kondoo, au nguo, au kitu chochote kilichopotea ambacho kila mumoja anadai kwamba ni chake, wale wanaobishana wataletwa mbele ya Mungu. Yule ambaye Mungu ataamua kwamba amekosa, atamulipa mwenzake mara mbili. Mutu akimupatia mwenzake punda, ngombe, kondoo au nyama mwingine yeyote amutunzie na nyama yule akikufa au akipelekwa bila mutu yeyote kushuhudia, kiapo mbele ya Yawe kitaamua kati yao, kwa kuonyesha kwamba yule aliyepewa hakuiba mali ya mwenzake. Mwenye nyama yule atakubali kile kiapo na yule mwenzake hatalipa malipo yoyote. Lakini kama aliibiwa kwake, anapaswa kumulipa mwenye naye. Kama yule nyama aliraruliwa na nyama wa pori, yule mutu aliyekuwa amepewa anapaswa kumuleta kama ushuhuda. Hatalipa malipo yoyote kwa ajili ya nyama aliyeraruliwa na nyama wa pori. Mutu akiazima nyama kwa mwenzake, kisha nyama yule akaumia au akakufa wakati mwenye naye hayuko, aliyeazima nyama yule anapaswa kumulipa kwa ukamilifu. Lakini kama mwenye naye alikuwa pale, basi aliyemwazima hatalipa kitu chochote. Kama alikuwa ni nyama aliyeazimwa, mwenye naye atakubali tu bei ya kuazima. Mutu akimutongoza binti ambaye hajachumbiwa, akilala naye, hakika atalipa mali na kumwoa binti yule. Baba wa yule binti akikataa kabisa kumwoesha binti yake, mutu yule atalipa feza ya mali inayostahili binti anayekuwa bikira. Usimwache mwanamuke muchawi aishi. Anayezini na nyama hakika atauawa. Anayemutolea mungu mwingine sadaka pahali pa Yawe pekee, lazima aangamizwe kabisa. Musimwonelee mugeni wala kumutesa, maana nanyi vilevile mulikuwa wageni katika inchi ya Misri. Musimutese mujane au yatima. Kama mukiwatesa wale, nao wakinililia, hakika nitakisikiliza kilio chao, na hasira yangu itawaka, nami nitawaua ninyi kwa upanga, na wake zenu watakuwa wajane na watoto wenu wayatima. Ukimukopesha feza mutu yeyote kati ya watu wangu wanaokuwa wamasikini, usikuwe kwake kama mudai, wala usimulipishe faida. Ukitwaa nguo ya mwenzako kama rehani, lazima umurudishie mbele ya jua kutua, kwa sababu hiyo ndiyo nguo yake ya pekee; ndiyo atakayojifunika nayo. Au unazani atalalia nini? Akinililia nitamusikiliza, maana mimi ni mwenye huruma. Usimutukane Mungu, wala kumulaani mukubwa wa watu wako. Usikawie kunitolea sehemu yangu kutokana na wingi wa mazao yako na divai yako. Mutanipa wazaliwa wenu wa kwanza wanaume. Mutafanya vile vile juu ya wazaliwa wa kwanza wa ngombe na kondoo wenu. Mutamwacha kila muzaliwa wa kwanza na mama yake kwa siku saba na siku ya nane mutanitolea. Ninyi mutakuwa watu waliotakaswa kwa ajili yangu. Kwa hiyo hamutakula nyama ya nyama aliyeuawa na nyama wa pori. Nyama hiyo mutaitupia imbwa. Usitoe habari za uongo. Usishirikiane na mutu mwovu kwa kuwa mushuhuda mubaya. Usifuate watu wengi kwa kutenda ubaya. Wala wakati wa kukata maneno, usishuhudie kufuatana na watu wengi kwa kupotosha haki. Usikuwe na upendeleo katika mashitaki ya masikini. Ukimukuta ngombe au punda wa adui yako amepotea, utamurudishia mwenye naye. Ukimwona punda wa mutu anayekuchukia ameanguka na muzigo wake, umusaidie mutu yule kumusimamisha punda wake, wala usimwache na kwenda zako. Usipotoshe haki masikini anayostahili katika mashitaki yake. Ujitenge mbali na mashitaki ya uongo wala usiwaue wasiokuwa na kosa na wenye haki, maana mimi sitamusamehe mutu mwovu. Usipokee kituliro, maana kituliro kinapofusha wakubwa na kupotosha mambo ya wenye haki. Usimutese mugeni. Ninyi munajua hali ya kuwa mugeni, maana mulikuwa wageni katika inchi ya Misri. Kwa muda wa miaka sita utapanda mashamba yako na kuvuna mazao yake. Lakini katika mwaka wa saba, utayaacha mashamba yako bila kupanda mbegu, kusudi wamasikini kati ya watu wako wapate chakula kilichobakia mule na nyama wa pori wakule. Utafanya vile vile katika shamba lako la mizabibu na la mizeituni. Kwa siku sita utafanya kazi zako, lakini siku ya saba utapumzika, kusudi ngombe wako na punda wako vilevile wapate kupumzika, na watoto wa mujakazi wako na wageni wapate kustarehe. Ushike mambo yote niliyokuambia. Usiyataje hata kidogo majina ya miungu mingine, hayo yasisikilike katika kinywa chako. Mara tatu kila mwaka mutafanya sikukuu kwa heshima yangu. Mutafanya sikukuu ya Mikate Isiyotiwa Chachu kama vile nilivyowaagiza. Mutakula mikate isiyotiwa chachu kwa siku saba wakati uliopangwa katika mwezi wa Abibu, kwa sababu katika mwezi ule mulitoka Misri. Mutu yeyote asikuje mbele yangu mikono mitupu. Mutafanya sikukuu ya mavuno ya kwanza ya kazi zenu na ya mavuno ya mashamba yenu. Mutafanya sikukuu ya kukusanya mavuno mwisho wa mwaka munapokusanya mazao ya kazi zenu. Mara tatu kwa mwaka wanaume wote watakusanyika mbele ya Bwana wenu, Yawe. Usinitolee damu ya sadaka yangu pamoja na mukate uliotiwa chachu, wala usiyaache mafuta ya sikukuu yangu yabaki mpaka asubui. Mazao ya kwanza ya shamba lako utayaleta katika nyumba yangu mimi Yawe, Mungu wako. Usipike mwana-kondoo au mwana-mbuzi katika maziwa ya mama yake. Muangalie, mimi ninamutuma malaika awatangulie katika safari kusudi awalinde na kuwafikisha katika inchi niliyowatayarishia. Musikilize na kutii maneno atakayosema, wala musimwasi. Hatawasamehe uasi wenu maana nimemutuma kwa jina langu. Lakini mukimusikiliza kwa uaminifu na kufanya yote anayosema, mimi nitakuwa adui wa waadui zenu na mupinzani wa wapinzani wenu. Malaika wangu atakapowaongoza na kuwafikisha katika inchi ya Waamori, Wahiti, Waperizi, Wakanana, Wahivi na Wayebusi, nami nitawaangamiza wale wote. Musiiname mbele ya miungu yao kuiabudu, wala kuitumikia, wala musiige mambo yao. Lakini mutawaangamiza kabisa na kuvunjavunja nguzo zao. Mutanitumikia mimi Yawe, Mungu wenu, nami nitawabariki kwa chakula na maji na kuondoa magonjwa kati yenu. Hakutakuwa mwanamuke yeyote atakayepoteza mimba wala kuwa tasa katika inchi yenu. Nami nitawajalia maisha marefu. Nitapeleka kitisho mbele yenu na kuwavuruga watu wote mutakaowafikia. Waadui zenu nitawafanya wageuke na kuwakimbia. Nitatuma nyuki mbele yenu ambazo zitawafukuza Wahivi, Wakanana na Wahiti. Sitawaondoa watu wale katika mwaka mumoja, inchi isibakie tupu na nyama wa pori wasiongezeke sana na kuwazidia nguvu. Lakini nitawaondoa kidogokidogo mpaka pale mutakapoongezeka na kurizi ile inchi. Mipaka ya inchi yenu itakuwa kutoka bahari Nyekundu mpaka bahari ya Mediteranea na kutoka jangwa mpaka muto Furati. Nitawatia wakaaji wa inchi ile katika mikono yenu, nanyi mutawafukuza wawaondokee. Musifanye agano lolote nao, wala na miungu yao. Musiwaruhusu waishi katika inchi yenu wasiwasukume kutenda zambi mbele yangu. Maana kama mukitumikia miungu yao, hakika ile itakuwa mutego wa kuwanasa. Yawe akamwambia Musa: Mukuje kwangu, wewe Haruni, Nadabu na Abihu, pamoja na wazee makumi saba wa Israeli, muniabudu kwa mbali. Wewe Musa peke yako ndiwe utakayenikaribia, lakini wengine wasikuje karibu na Waisraeli wasipande juu ya mulima pamoja nawe. Basi, Musa akaenda na kuwaambia watu wote maneno na maagizo yote Yawe aliyomwambia. Watu wote wakajibu kwa sauti moja: Mambo yote Yawe aliyosema, tutayafanya. Musa akaandika maagizo yote ambayo Yawe alimupa. Kisha akaamuka asubui mapema, akajenga mazabahu chini ya mulima na kusimamisha nguzo kumi na mbili kulingana na hesabu ya makabila kumi na mbili ya Israeli. Kisha akatuma vijana wa watu wa Israeli wamutolee Yawe sadaka za kuteketezwa kwa moto na kumuchinjia sadaka za amani za ngombe. Musa akachota nusu ya damu ya nyama wale na kuiweka katika mabeseni na nusu ingine akainyunyiza juu ya mazabahu ile. Kisha akatwaa kitabu cha agano la Yawe, akakisoma mbele ya watu, nao wakasema: Yale yote Yawe aliyoyasema tutayafanya, nasi tutakuwa watiifu. Musa akatwaa ile damu na kuwanyunyizia watu, akisema: Hii ndiyo damu ya agano ambalo Yawe amefanya nanyi kufuatana na maneno haya yote. Kisha Musa, Haruni, Nadabu na Abihu na wazee makumi saba wa Israeli wakapanda juu ya mulima, wakamwona Mungu wa Israeli. Chini ya miguu yake kulikuwa kitu kama sakafu ya mawe ya yakuti samawi, kikiwa safi kama mbingu inayoangaa. Na Mungu hakuwazuru wale viongozi wa watu wa Israeli. Walimwona Mungu, wakakula na kunywa. Yawe akamwambia Musa: Kuja kwangu juu kwenye mulima, ungoje kule. Mimi nitakupa vibao vya mawe vyenye sheria na amri nilizoandika kwa ajili ya kuwafundisha Waisraeli. Basi, Musa akaondoka pamoja na Yoshua, mutumishi wake, akaenda kwenye mulima wa Mungu. Musa aliwaambia wale wazee: Mutungojee hapa mpaka tutakapowarudilia. Haruni na Huri wako pamoja nanyi. Yeyote anayekuwa na tatizo awaendee wao. Basi, Musa akaenda kwenye mulima na wingu likafunika mulima. Utukufu wa Yawe ukatua juu ya mulima Sinai na wingu likafunika mulima kwa muda wa siku sita. Siku ya saba Mungu akamwita Musa kutoka katikati ya lile wingu. Utukufu wa Yawe ukaonekana mbele ya macho ya watu wa Israeli kama moto unaowaka juu ya mulima. Musa akaingia ndani ya lile wingu, akapanda kwenye mulima. Alikaa kule kwa muda wa siku makumi ine, muchana na usiku. Yawe akamwambia Musa: Uwaambie Waisraeli wanipe michango ya matoleo. Utapokea matoleo kutoka kwa mutu yeyote atakayetoa kwa moyo safi. Utapokea matoleo haya: zahabu, feza, shaba, sufu ya samawi, ya zambarau na nyekundu, kitani safi iliyosokotwa na manyoya ya mbuzi; ngozi za kondoo dume zilizotiwa rangi nyekundu, ngozi za mbuzi, mbao za mujohoro, mafuta kwa ajili ya taa, viungo kwa ajili ya mafuta ya kupakaa na kwa ajili ya ubani wenye harufu nzuri, mawe ya sardoniki, na mawe mengine kwa ajili ya mapambo ya kizibao cha kuhani na kifuko cha kifua. Vilevile Waisraeli watanitengenezea hema takatifu, kusudi niweze kukaa kati yao. Utatengeneza hema hiyo na vifaa vyake kulingana na mufano nitakaokuonyesha. Waisraeli watengeneze sanduku la mbao za mujohoro, lenye urefu wa sentimetre mia moja na kumi, upana sentimetre makumi sita na sita, na urefu kwenda juu sentimetre makumi sita na sita. Utapaka sanduku lile zahabu safi ndani na inje na kulifanyia ukingo wa zahabu pande zote. Kisha utalitengenezea pete ine na kuzitia kwenye miguu yake, kila muguu pete moja. Utachonga miti ya mujohoro na kuipakaa zahabu. Miti ile utaipitisha katika pete zinazokuwa kwa pande mbili za sanduku, kwa ajili ya kulibeba. Miti ile itabaki siku zote katika pete. Isitolewe wakati wowote. Ndani ya sanduku hilo utaweka vibao vya mawe vya agano. Kisha utatengeneza kiti cha rehema cha zahabu safi, urefu wake sentimetre mia moja na kumi, na upana wake sentimetre makumi sita na sita. Utatengeneza vilevile mufano wa makerubi wawili kwa kufua zahabu, uwaweke kwenye miisho miwili ya kiti kile; kerubi mumoja kwa mwisho mumoja na kerubi mwingine kwa mwisho mwingine. Uwaweke makerubi wale kwenye miisho ya kiti kile, lakini wakuwe kitu kimoja na kile kiti. Makerubi wale wataelekeana, mabawa yao yakikunjuka kukifunika kiti cha rehema. Nyuso zao zitaelekea kiti kile. Ndani ya sanduku utaweka vibao vya amri na kuweka kiti cha rehema juu yake. Mimi nitakutana nawe pale. Kutoka juu ya kiti kile cha rehema katikati ya makerubi wale wanaokuwa juu ya Sanduku la Agano, nitazungumuza nawe na kukupa amri zote kwa ajili ya Waisraeli. Utatengeneza meza ya mbao za mujohoro yenye urefu wa sentimetre makumi nane na nane, upana sentimetre makumi ine na ine na urefu kwenda juu sentimetre makumi sita na sita. Ile meza utaipakaa zahabu safi na kuizungushia ukingo wa zahabu. Kisha utaizungushia ubao wenye upana wa sentimetre makumi sita na sita na utaufanyia vilevile ukingo wa zahabu. Utaitengenezea pete ine za zahabu na kuzitia kwenye pembe zake kwenye miguu yake. Pete hizo zitakuwa karibu na ule ubao wa kuzunguka meza na zitakuwa za kuingizia ile miti ya kubebea ile meza. Utachonga miti ya mujohoro na kuipakaa zahabu. Miti itakuwa ya kubebea ile meza. Utatengeneza kwa ajili yake: sahani na vikombe vya kuwekea ubani na vilevile makopo na bakuli za kumiminia sadaka za kinywaji. Ufanye vyombo hivyo vyote kwa zahabu safi. Meza hiyo utaiweka mbele ya Sanduku la Agano na juu ya meza ile utaweka ile mikate muliyonitolea. Mikate ile itakuwa siku zote mbele yangu. Utatengeneza kinara cha taa kwa zahabu safi. Tako lake na muti wa kile kinara vitakuwa kitu kimoja, vilevile na vikombe vyake. Mafundo yake na maua yake, vyote vitafuliwa kwa kipande kimoja tu cha zahabu. Matawi sita yatatokeza kila upande wa muti wake, matawi matatu upande mumoja na matawi matatu upande mwingine. Katika kila tawi kutakuwa vikombe vitatu mufano wa maua ya lozi, kila kimoja na kifundo chake na ua lake. Na katika muti kutakuwa vikombe vine mufano wa maua ya lozi, pamoja na vifundo vyake na maua yake. Na kutakuwa kifundo kila pahali matawi mawilimawili yanapotokea kufuatana na yale matawi sita yanayotokea kwa kile kinara. Vifundo hivyo na matawi yake yatakuwa kitu kimoja na kinara kile na chote kitafuliwa kwa zahabu safi. Utatengeneza vilevile taa saba kwa ajili ya kinara kile na kuziweka juu yake kusudi ziangaze kwa mbele. Tengeneza vilevile koleo zake na visahani vyake kwa zahabu safi. Utatumia kilo makumi tatu na tano za zahabu safi kwa kutengeneza kinara kile na vifaa vyake. Hakikisha kwamba umevitengeneza kwa mufano ulioonyeshwa kule juu ya mulima. Zaidi ya hayo yote, utatengeneza hema takatifu kwa mapazia kumi ya kitani safi iliyosokotwa, na kwa sufu ya rangi ya samawi, zambarau na nyekundu. Mapazia hayo utayapamba kwa makerubi waliochorwa. Kila pazia litakuwa na urefu wa metre kumi na mbili na upana wa metre mbili. Mapazia hayo yakuwe ya kipimo kimoja. Utaunganisha mapazia matano yakuwe kipande kimoja na mapazia mengine matano yakuwe kipande cha pili. Utashonea kamba za rangi ya samawi kwenye upindo wa pazia la mwisho la kipande cha kwanza. Vilevile utashonea kamba kwa mwisho wa pindo la inje la kipande kingine cha pazia. Utatia kamba makumi tano katika pazia moja na kamba zingine makuni tano kwenye utepe wa pazia la pili, kamba zote zielekeane. Kisha utatengeneza vifungio makumi tano vya zahabu kwa kuunganishia vile vipande viwili vya mapazia, hivyo hema litakuwa kitu kimoja. Vilevile utatengeneza kifuniko cha hema kwa mapazia kumi na moja ya manyoya ya mbuzi. Kila pazia litakuwa na urefu wa metre kumi na tatu na upana wa metre mbili. Mapazia yote yale kumi na moja yatakuwa na kipimo kilekile. Utaunga mapazia matano pamoja na mapazia sita pamoja. Pazia la sita utalikunja mara mbili mbele ya hema. Kisha utafanya kamba makumi tano kwenye upindo wa pazia la mwisho la kipande cha kwanza na kamba makumi tano kwenye upindo wa pazia la mwisho la kipande cha pili. Utatengeneza vifungio makumi tano vya shaba na kuviingiza katika zile kamba makuni tano kwa kuunganishia vile vipande viwili vya mapazia na hivyo kufanya pazia moja la hema. Ile nusu ya pazia iliyobaki utaitundika upande wa nyuma wa hema. Nusu metre ya urefu wa mapazia iliyokuwa ya zaidi utaikunja ininginie pande zote kwenye mbavu ya hema kwa kulifunika. Utatengeneza vilevile kifuniko kingine cha hema kilichofanywa kwa ngozi laini ya kondoo dume na ngozi laini ya mbuzi. Utatengeneza mbao za mujohoro za kusimama wima kwa ajili ya hema. Kila ubao utakuwa na urefu wa metre ine na upana wa sentimetre makumi sita na sita. Kila ubao utakuwa na ndimi mbili za kuunganishia. Utazifanyia mbao zote ndimi mbili. Basi, utatengeneza zile mbao za hema hivi: mbao makumi mbili kwa ajili ya upande wa kusini, na vikalio makumi ine vya feza chini ya zile mbao makumi mbili, vikalio viwili chini kwa kila ubao kwa kushikilia zile ndimi zake mbili na vikalio viwili vikuwe chini ya ubao mwingine kwa kushikilia zile ndimi zake mbili. Upande wa kaskazini wa hema, utatengeneza mbao makumi mbili, na vikalio vyake makumi ine vya feza, vikalio viwili chini ya kila ubao. Kwa upande wa nyuma, unaokuwa kwa upande wa magaribi wa hema, utatengeneza mbao sita. Utatengeneza vilevile mbao mbili kwa ajili ya pembe za hema upande wake wa nyuma. Mbao zile za pembeni ziachane chini lakini zishikamanishwe kwa juu kwenye pete ya kwanza. Mbao zote za pembeni zifanywe vile vile kusudi zifanye pembe mbili. Hivyo kutakuwa mbao nane pamoja na vikalio vyake kumi na sita vya feza: vikalio viwili chini ya kila mbao na vikalio viwili chini ya ubao mwingine. Utatengeneza miti ya mujohoro; miti tano kwa ajili ya mbao za upande mumoja wa hema, na miti tano kwa ajili ya upande wa pili wa hema, na miti tano kwa ajili ya mbao za upande wa nyuma wa hema, kwa upande wa magaribi. Muti wa katikati uliofika nusu ya jengo la hema utapenya katikati toka mwisho huu mpaka mwisho mwingine wa hema. Mbao zote utazipakaa zahabu na kuzifanyia pete za zahabu zitakazoshikilia ile miti, ambazo vilevile utazipakaa zahabu. Hivyo utalitengeneza hema hilo kulingana na mufano niliokuonyesha juu ya mulima. Utatengeneza pazia la nyuzi za rangi ya samawi, zambarau na nyekundu na kitani safi iliyosokotwa. Juu ya pazia lile utachora kwa ufundi sanamu za makerubi. Utalitundika pazia kwenye nguzo ine za mujohoro zilizopakwa zahabu, zenye vifungio vya zahabu na vikalio vine vya feza. Utatundika pazia lile kwenye vifungio, kisha ulete lile Sanduku la Agano mule ndani, nyuma ya pazia lile. Pazia lile litatenga Pahali Patakatifu na Pahali Patakatifu Sana. Ndani ya Pahali Patakatifu utaweka kile kiti cha rehema juu ya Sanduku la Agano. Ile meza ya mujohoro utaiweka upande wa inje wa pazia lile, na kile kinara cha taa utakiweka upande wa kusini wa hema, kikielekeana na meza. Meza ile itakuwa upande wa kaskazini. Kwa ajili ya mulango wa hema utatengeneza pazia zito kwa sufu ya rangi ya samawi, zambarau na nyekundu, na kitani safi iliyosokotwa, na kuchorwa vizuri. Vilevile utatengeneza nguzo tano za mujohoro na kuzipakaa zahabu. Nguzo hizo zitakuwa na vifungio vya zahabu, na kila moja itakuwa na tako la shaba. Utatengeneza mazabahu kwa mbao za mujohoro. Mazabahu ile itakuwa ya muraba, urefu wake metre mbili na sentimetre makumi mbili, na upana wake metre mbili na sentimetre makumi mbili. Urefu kwenda juu utakuwa metre moja na sentimetre makumi mbili. Katika kila pembe ya mazabahu ile utatengeneza upembe ambao utakuwa umeundwa kutokana na mazabahu yenyewe. Mazabahu ile yote utaipakaa shaba. Utaitengenezea vyombo vyake: vyungu vya kuwekea majivu, majembe, na mabeseni, na kanya na visahani vya kutwalia moto. Vyombo vyake vyote utavitengeneza kwa shaba. Kisha utatengeneza wavu wa shaba wenye pete ine za shaba kwenye pembe zake ine. Wavu ule utauweka kwenye ukingo wa mazabahu upande wa chini kusudi ufike katikati ya mazabahu. Utatengeneza vilevile miti ya mujohoro ya kubebea mazabahu, nayo utaipakaa shaba. Miti ile itaingizwa kwenye zile pete kila upande wa mazabahu wakati wa kuibeba. Utatengeneza mazabahu kwa mbao, ikuwe wazi ndani, kulingana na mufano niliokuonyesha juu ya mulima. Utatengeneza kiwanja cha hema la mukutano. Kwa upande wa kusini wa kiwanja kutakuwa nguo zilizotengenezwa kwa kitani safi iliyosokotwa ambazo zitakuwa na urefu wa metre makumi ine na ine kwa upande mumoja. Nguo zile zitashikiliwa na nguzo makumi mbili za shaba zenye vikalio vya shaba. Lakini vifungio vya nguzo zile na kamba zake vitakuwa vya feza. Vilevile upande wa kaskazini, urefu wa nguo utakuwa metre makumi ine na ine, na nguzo zake makumi mbili za shaba, lakini vifungio vya nguzo na kamba zake vitakuwa vya feza. Upande wa magaribi wa kiwanja utakuwa na nguo yenye urefu wa metre makumi mbili na mbili na nguzo zake kumi na vikalio vyake kumi. Upande wa mashariki kunakokuwa mulango, kiwanja kitakuwa na upana wa metre makumi mbili na mbili. Nguo ya upande mumoja wa mulango itakuwa na upana wa metre sita na nusu, pamoja na nguzo tatu na vikalio vyake vitatu. Vilevile katika upande wa pili wa mulango nguo itakuwa metre sita na nusu, pamoja na nguzo tatu na vikalio vyake vitatu. Mulango wenyewe wa kiwanja utakuwa na pazia zito lenye urefu wa metre tisa, lililotengenezwa kwa sufu ya rangi ya samawi, zambarau na nyekundu, na kitani safi iliyosokotwa, na kuchorwa vizuri. Pazia lile litashikiliwa na nguzo ine zenye vikalio vine. Nguzo zote kuzunguka kiwanja zitashikamanishwa kwa fito za feza. Vifungio vyake vitakuwa vya feza na vikalio vyake vitakuwa vya shaba. Kiwanja kile kitakuwa na urefu wa metre makumi ine na ine, upana wa metre makumi mbili na mbili, na urefu kwenda juu wa metre mbili na sentimetre makumi mbili. Nguo zake zitakuwa za kitani safi na vikalio vyake vya shaba. Vyombo vyote vya hema takatifu vya matumizi ya kila aina, pamoja na misumari vyote na hata vile vya kiwanja, vitakuwa vya shaba. Utawaamuru Waisraeli wakuletee mafuta safi kwa ajili ya taa, kuwe taa inayowaka siku zote. Hiyo itakuwa ndani ya hema la mukutano inje ya pazia lile mbele ya Sanduku la Agano na Haruni na wana wake wataitunza mbele yangu tangu magaribi mpaka asubui. Sharti hili lifuatwe siku zote na Waisraeli wote, kizazi kwa kizazi. Nawe Musa umulete kwangu Haruni ndugu yako, pamoja na wana wake: Nadabu, Abihu, Eleazari na Itamari. Utawachagua kati ya Waisraeli, kusudi wanitumikie kama vile makuhani. Utamushonea ndugu yako Haruni nguo takatifu kusudi apate kuonekana mwenye utukufu na muzuri. Uwaagize wafundi wote ambao nimewapa maarifa wamutengenezee Haruni nguo kusudi atakaswe kwa ajili ya kazi ya ukuhani. Uwaambie wamutengenezee vitu hivi: kifuko cha kifua, kizibao, kanzu, na ingine yenye kupambwa vizuri, kofia na mukaba. Ndugu yako Haruni na wana wake watavaa nguo zile kusudi wanitumikie kama vile makuhani. Hao wafundi watatumia sufu ya rangi ya samawi, zambarau na nyekundu, na nyuzi za zahabu na kitani safi iliyosokotwa. Watatengeneza kizibao cha kuhani kwa nyuzi za zahabu na sufu ya rangi ya samawi, zambarau na nyekundu, na kitani safi iliyosokotwa, na kupambwa vizuri. Kitakuwa kamba mbili za kukifungia juu ya mabega zilizoshonewa kwenye incha zake mbili. Mukaba wa kukishikia utatengenezwa kwa vifaa hivyohivyo: kwa nyuzi za zahabu, sufu ya samawi, zambarau na nyekundu, na kitani safi iliyosokotwa na kuwa kitu kimoja na kizibao kile. Kisha utatwaa mawe mawili ya sardoniki ambayo utachora juu yake majina ya wana wa Israeli. Majina sita katika jiwe la kwanza, na majina sita yaliyobakia katika jiwe la pili, majina yafuatane kadiri ya kuzaliwa kwao. Utayachora majina yale juu ya yale mawe kama vile muchoraji anavyochora muhuri, kisha uyaingize katika kingo za zahabu. Mawe hayo mawili yatawekwa juu ya mikaba ya kizibao kama vile ukumbusho wa makabila kumi na mawili ya Israeli. Hivyo Haruni atavaa majina hayo juu ya mabega yake mbele yangu mimi Yawe kama vile ukumbusho. Utayatengenezea kingo mbili za zahabu, na mikufu miwili ya zahabu safi iliyosokotwa kama kamba. Utafunga mikufu ile kwenye zile kingo. Utatengeneza kifuko cha kifua cha maamuzi. Kitengenezwe kwa ufundi sawa vile kile kizibao kilivyotengenezwa: kwa zahabu, kwa sufu ya rangi ya samawi, zambarau na nyekundu, na kitani safi iliyosokotwa. Kifuko hicho ambacho kimekunjwa kitakuwa cha muraba, sentimetre makumi mbili na mbili. Kitapambwa kwa mistari ine ya mawe ya bei kali. Mustari wa kwanza utakuwa wa akiki, topazi na almasi nyekundu; mustari wa pili utakuwa wa zumaridi, yakuti samawi na almasi; mustari wa tatu utakuwa wa yasinto, akiki nyekundu na ametisto; na mustari wa ine utakuwa wa zabarajadi, shohamu na yaspi. Yote yatatiwa kwenye kingo za zahabu. Basi, kutakuwa mawe kumi na mawili yaliyochorwa majina kumi na mawili ya wana wa Israeli. Kila moja litakuwa kama muhuri, kwa kusimamia makabila yale kumi na mawili. Kwa ajili ya kifuko kile cha kifua, utatengeneza mikufu ya zahabu safi iliyosokotwa kama kamba. Vilevile utatengeneza pete mbili za zahabu kwa ajili ya kifuko cha kifua na kuzitia kwenye incha mbili za kifuko hicho, na mikufu miwili ya zahabu uifunge kwenye pete zile za kifuko cha kifua. Zile incha mbili za mukufu wa zahabu utazishikamanisha kwenye zile kingo mbili za kile kifuko kusudi zishikamane na kipande cha mabega cha kizibao upande wa mbele. Vilevile utatengeneza pete mbili za zahabu na kuzitia kwenye incha mbili za chini upande wa ndani wa kifuko cha kifua karibu na kizibao. Kisha utatengeneza pete zingine mbili za zahabu na kuzitia mbele katika incha za chini za vipande vya kizibao, pahali kizibao kinapoungana na mukaba uliofumwa kwa ufundi. Kifuko cha kifua kitafungwa kwenye kizibao kwa kufunganisha pete zake na kizibao kwa kamba ya rangi ya samawi, kusudi kifuko kile cha kifua kisiregee lakini kikalie ule mukaba uliofumwa kwa ufundi. Haruni anapoingia Pahali Patakatifu, atavaa kifuko cha shauri ambacho juu yake kulichorwa majina ya makabila ya wana wa Israeli. Kwa namna hiyo mimi Yawe sitawasahau ninyi hata kidogo. Kwenye kifuko hicho utatia mawe ya shauri yaninginie kwenye kifua cha Haruni kila mara anapokuja mbele yangu. Wakati ule anapaswa kila mara kuvaa kifuko kile, kusudi aweze kutambua mapenzi yangu juu ya Waisraeli. Utashona kanzu ya kuvalia chini ya kizibao ikiwa yote ya rangi ya samawi. Kanzu ile itakuwa na nafasi ya kupitishia kichwa katikati na nafasi hiyo itazungushiwa utepe uliofumwa kusudi isichanike. Kwenye upindo wake wa chini, kuzunguka pande zote, itapambwa kwa makomamanga ya rangi ya samawi, zambarau na nyekundu. Kutakuwa vilevile kengele za zahabu kati ya hayo makomamanga: komamanga, kengele, komamanga, kengele, kuizunguka kanzu yote. Haruni atavaa kanzu ile kwa kutimiza kazi yake ya kuhani na sauti yake itasikilika wakati anapoingia Pahali Patakatifu mbele yangu na wakati anapotoka, kengele hizo zitasikilika, naye hatauawa. Kisha, utatengeneza bamba la zahabu safi na kuchora juu yake maneno haya kama vile mutu anavyochora muhuri: Takatifu kwa ajili ya Yawe. Utalifungia bamba lile mbele ya kofia kwa mukaba wa rangi ya samawi. Haruni atavaa bamba lile kwenye paji la uso wake. Kwa njia ya bamba lile atabeba mashitaki ya makosa ambayo Waisraeli wanaweza kuwa wamefanya katika kunitolea sadaka takatifu, nami nitakubali sadaka zao. Utamutengenezea Haruni kanzu iliyochorwa kwa kitani safi na kumufumia kofia ya kitani safi na mukaba uliopambwa vizuri. Utawatengenezea wana wa Haruni kanzu, mikaba na kofia kusudi waonekane wana utukufu na uzuri. Utamuvalisha ndugu yako Haruni na wana wake nguo zile, kisha uwapakae mafuta na kuwawekea mikono kwa kuwatakasa wanitumikie kama vile makuhani. Vilevile utawashonea makapitula za kitani zitakazowafunika tangu kwenye kiuno mpaka kwenye mapaja, kusudi wafunike uchi wao. Haruni na wana wake watavaa makapitula hizo kila mara wanapoingia katika hema la mukutano, au wanapokaribia kwenye mazabahu, kufanya kazi za makuhani katika Pahali Patakatifu. Kwa njia hiyo hawataonyesha uchi wao na kuwa na hatari ya kuuawa. Hilo ni sharti la kufuatwa siku zote kwa Haruni na wazao wake. Haya ndiyo mambo utakayowafanyia Haruni na wana wake kwa kuwatakasa wapate kunitumikia kama vile makuhani. Utatwaa mwana-ngombe dume na kondoo dume wawili wasiokuwa na kilema, mikate isiyotiwa chachu, maandazi yasiyotiwa chachu yaliyopondwa kwa mafuta, na mikate myembamba isiyotiwa chachu, lakini iliyopakwa mafuta. Vyote hivi vikuwe vimetengenezwa kwa unga laini wa ngano. Kisha uweke hiyo mikate ndani ya kikapu kimoja na kunitolea wakati mumoja na yule mwana-ngombe dume na wale kondoo dume wawili. Kisha uwapeleke Haruni na wana wake kwenye mulango wa hema la mukutano na kuwanawisha. Kisha utatwaa zile nguo za kikuhani umuvalishe Haruni: koti, kanzu, kizibao, kifuko cha kifua, na kumufunga ule mukaba uliofumwa kwa ufundi. Tena utamuvalisha ile kofia juu ya kichwa na kuweka juu ya ile kofia ile taji takatifu. Kisha kufanya hivyo, utatwaa yale mafuta ya kupakaa, umumiminie Haruni juu ya kichwa chake kwa kumutakasa. Kisha utawaleta wana wa Haruni na kuwavalisha vizibao. Utawafunga mikaba katika viuno na kuwavalisha kofia zao. Hivi ndivyo utakavyowatakasa Haruni na wana wake kuwa makuhani. Hao watakuwa makuhani siku zote kwa ajili ya sharti la siku zote. Kisha utamuleta yule mwana-ngombe dume mbele ya hema la mukutano. Haruni na wana wake wataweka mikono yao juu ya kichwa cha mwana-ngombe yule na kumuchinja mbele ya Yawe, kwenye mulango wa hema la mukutano. Utatwaa sehemu ya damu na kuipakaa kwenye pembe za mazabahu kwa kidole chako, na damu yote inayobaki utaimwanga chini ya mazabahu. Halafu utatwaa mafuta yote yanayofunika matumbotumbo, sehemu bora ya maini pamoja na figo mbili na mafuta yake, uviteketeze vyote juu ya mazabahu. Lakini nyama ya ngombe dume yule pamoja na ngozi na mavi yake utavitwaa na kuviteketeza inje ya kambi yenu. Hii itakuwa sadaka ya kuondoa zambi. Kisha utatwaa mumoja wa wale kondoo dume na kumwambia Haruni na wana wake waweke mikono yao juu ya kichwa chake. Nawe utamuchinja na damu yake utairushia juu ya mazabahu pande zake zote. Halafu utamukata yule kondoo vipandevipande. Utasafisha matumbotumbo yake na miguu yake, uviweke vyote pamoja na kichwa na vipande vingine. Kisha utamuteketeza kondoo muzima juu ya mazabahu kwa kunitolea sadaka ya kuteketezwa. Harufu ya sadaka inayotolewa kwa moto itanipendeza mimi Yawe. Utatwaa yule kondoo mwingine, naye Haruni na wana wake wataweka mikono yao juu ya kichwa chake. Nawe utamuchinja na kutwaa sehemu ya damu na kumupakaa Haruni na wana wake kwenye incha za masikio yao ya kuume na vidole gumba vya mikono yao ya kuume, na vidole gumba vya miguu yao ya kuume. Damu inayobaki utairushia juu ya mazabahu pande zake zote. Kisha utatwaa sehemu ya damu inayokuwa juu ya mazabahu pamoja na yale mafuta ya kupakaa umunyunyizie Haruni na nguo yake, uwanyunyizie vilevile wana wake na nguo zao. Haruni na wana wake watakuwa wametakaswa kwa ajili yangu pamoja na nguo zao zote. Kisha utatwaa mafuta ya yule kondoo dume: mukia wake, mafuta yanayofunika matumbotumbo na sehemu bora ya maini, figo zake mbili na mafuta yake, pamoja na paja la kuume. (Kondoo yule ni kondoo wa utakaso.) Kutoka katika kile kikapu cha mikate isiyotiwa chachu kinachokuwa mbele yangu mimi Yawe, utatwaa mukate mumoja na andazi moja lililotiwa mafuta na mukate mwembamba mumoja. Vyote hivi utavipatia Haruni na wana wake nao wataviinua juu kuwa kitambulisho cha kunitolea sadaka mimi Yawe. Kisha utavitwaa tena kutoka mikono yao na kuviteketeza juu ya mazabahu pamoja na ile sadaka ya kuteketezwa, vikuwe harufu nzuri itakayonipendeza mimi Yawe. Hiyo ni sadaka inayotolewa kwa moto. Kisha utatwaa kilali cha yule kondoo wa kumutakasa Haruni na kufanya kitambulisho cha kunitolea mimi Yawe. Nacho kitakuwa sehemu yako. Kuhani anapotakaswa, kilali na paja la kondoo dume wa utakaso vitaletwa na kutakaswa mbele yangu kwa kufanya kitambulisho cha kunitolea, navyo vitakuwa vya Haruni na wana wake. Hivyo siku zote Waisraeli watatwaa sehemu hizo kutoka katika sadaka zao za amani wanazonitolea mimi Yawe na kumupa Haruni na wana wake. Hiyo ni sadaka yao kwa Yawe. Kisha kufa kwa Haruni, nguo zake takatifu zitapewa kwa wana wake, nao watazivaa siku yao ya kupakwa mafuta na kuwekewa mikono. Mwana wa Haruni atakayekuwa kuhani pahali pa baba yake atavaa nguo zile siku saba katika hema la mukutano, kwa kutumika katika Pahali Patakatifu. Utatwaa nyama ya yule kondoo wa utakaso na kuitokotesha katika Pahali Patakatifu. Kisha utawapa Haruni na wana wake, nao wataikula kwenye mulango wa hema la mukutano pamoja na ile mikate iliyobakia katika kikapu. Watakula vitu hivyo vilivyotumika kwa utakaso na kwa ajili ya kuwafanyia upatanisho, lakini mutu mwingine asiruhusiwe kuvikula maana ni vitakatifu. Kama nyama yoyote au mikate hiyo itabakia mpaka asubui yake, basi utaiteketeza kwa moto. Isikuliwe maana ni kitu kitakatifu. Hivi ndivyo utakavyowatendea Haruni na wana wake kufuatana na yote yale niliyokuamuru. Utawatakasa kwa muda wa siku saba, na kila siku utatoa ngombe dume akuwe sadaka ya maondoleo ya zambi kwa kufanya upatanisho. Kwa kufanya hivyo utasafisha mazabahu, kisha utaimiminia mafuta kwa kuitakasa. Kwa siku saba utafanyia mazabahu upatanisho na kuitakasa. Nyuma ya hayo, mazabahu itakuwa takatifu kabisa na chochote kitakachoigusa kitakuwa kitakatifu. Kila siku, wakati wote unaokuja, utatolea sadaka juu ya mazabahu: wana-kondoo wawili wenye umri wa mwaka mumoja. Mwana-kondoo mumoja utamutoa sadaka asubui na mwingine magaribi. Pamoja na mwana-kondoo wa kwanza, utatoa kilo moja ya unga laini uliochanganywa na litre moja ya mafuta safi, na litre moja ya divai kama sadaka ya kinywaji. Vilevile na yule mwana-kondoo mwingine wa magaribi utamutolea sadaka pamoja na sadaka ya ngano na ya kinywaji kama vile ulivyofanya asubui. Harufu ya sadaka hiyo inayotolewa kwa moto itanipendeza mimi Yawe. Sadaka hii ya kuteketezwa itatolewa siku zote, kizazi kwa kizazi, mbele yangu mimi Yawe, mbele ya mulango wa hema la mukutano ambapo mimi nitakutana nanyi na kuongea nanyi. Hapo ndipo nitakapokutana na Waisraeli na utukufu wangu utapafanya pawe patakatifu. Hema la mukutano na mazabahu nitavifanya vitakatifu. Vilevile Haruni na wana wake nitawatakasa kusudi wanitumikie kama makuhani. Nitaishi kati ya Waisraeli, nami nitakuwa Mungu wao. Hapo ndipo watakapotambua kwamba mimi ni Yawe, Mungu wao, niliyewaleta kutoka katika inchi ya Misri, kusudi niishi kati yao. Mimi ni Yawe, Mungu wao. Utatengeneza mazabahu kwa mbao za mujohoro kusudi pawe pahali pa kufukizia ubani. Mazabahu hiyo ikuwe ya muraba, urefu na upana wake sentimetre makumi ine na tano, na urefu kwenda juu sentimetre makumi tisa. Pembe zake za juu zitatokeza zote zikiwa kitu kimoja na mazabahu yenyewe. Yote utaipakaa zahabu safi: upande wake wa juu, pande zake zote za ubavu na pembe zake. Vilevile utaizungushia ukingo wa zahabu. Utaitengenezea pete mbili za zahabu na kuzitia chini ya ukingo wake kwenye pande mbili zinazoelekeana. Hizo pete zitatumiwa kwa kushikilia miti wakati wa kuibeba. Miti hiyo ikuwe ya mujohoro na ipakwe zahabu. Mazabahu hiyo iwekwe mbele ya pazia kando ya Sanduku la Agano, mbele ya kiti cha rehema ambapo nitakutana nawe. Kila siku Haruni anapoingia kwa kutayarisha taa zinazokuwa pale, atafukiza ubani wenye harufu nzuri juu ya mazabahu hiyo. Tena atafukiza ubani wakati wa magaribi anapowasha taa. Sadaka hii ya ubani itatolewa siku zote bila kukoma katika vizazi vyenu vyote. Kwenye mazabahu hiyo, musifukize hata kidogo ubani usiokuwa mutakatifu, wala musitoe sadaka ya kuteketezwa, wala sadaka ya ngano, wala kumimina juu yake sadaka ya kinywaji. Haruni atafanya upatanisho juu ya pembe za mazabahu hiyo mara moja kwa mwaka. Ataifanyia upatanisho kwa damu ya sadaka ya maondoleo ya zambi mara moja kila mwaka katika vizazi vyenu vyote, maana mazabahu hiyo ni takatifu kabisa kwangu, mimi Yawe. Yawe akamwambia Musa: Kila mara utakapowahesabu Waisraeli, kila mumoja atatoa malipo kwa Yawe kwa ajili ya nafsi yake kusudi kusikuwe hasara kati yao wakati wa kuhesabiwa. Kila mumoja atakayehesabiwa anapaswa kulipa nusu ya shekeli kulingana na vipimo vya hema la mukutano. Hii ni sadaka yake atakayonitolea. Kila mumoja atakayehesabiwa, tangu umri wa miaka makumi mbili na zaidi, atanitolea sadaka hiyo. Tajiri asitoe zaidi wala masikini asitoe chini ya nusu ya shekeli wakati munaponitolea sadaka hiyo kwa kufanya upatanisho. Wewe utaipokea feza hiyo ya upatanisho kutoka kwa Waisraeli, nawe utaitumia kwa shuguli za kazi za hema takatifu, nayo ikuwe ni ukumbusho wa Waisraeli mbele yangu, malipo ya maisha yenu. Yawe akamwambia Musa: Utatengeneza birika la shaba kwa kuoga lenye tako la shaba, uliweke katikati ya hema la mukutano na mazabahu, na kutia maji ndani yake. Haruni na wana wake watatumia maji hayo kwa kunawa mikono na miguu, mbele ya kuingia kwenye hema la mukutano au kukaribia mazabahu kwa kunitolea sadaka mimi Yawe, sadaka za kuteketezwa kwa moto. Watafanya hivyo kusudi wasikufe. Wanapaswa kunawa mikono na miguu yao kusudi wasikufe. Hili ni sharti kwao siku zote, tangu Haruni na uzao wake, vizazi kwa vizazi. Yawe akamwambia Musa: Utatwaa viungo bora kabisa kama hivi: manemane ya maji kilo sita, mudalasini wenye harufu nzuri kilo tatu, miwa yenye harufu nzuri kilo tatu, na aina nyingine ya mudalasini kilo sita – vipimo hivyo vyote vikuwe kufuatana na vipimo vya hema takatifu. Twaa vilevile litre ine za mafuta. Kutokana na viungo hivyo utatengeneza mafuta matakatifu uyachanganye kama vile fundi wa manukato anavyofanya. Hayo yatatumika kwa kutakasa vitu. Kisha utamiminia hema la mukutano mafuta hayo, Sanduku la Agano, meza na vyombo vyake vyote, kinara cha taa na vyombo vyake, mazabahu ya kufukizia ubani, mazabahu ya sadaka za kuteketezwa kwa moto na vyombo vyake vyote, na birika na tako lake. Utavitakasa, kusudi vikuwe vitakatifu kabisa. Chochote kitakachogusa vifaa hivyo, kitakuwa kitakatifu. Kisha umupakae Haruni mafuta na wana wake na kuwatakasa kusudi wanitumikie kama vile makuhani. Uwaambie Waisraeli kwamba haya yatakuwa mafuta yangu matakatifu ya kupakaa katika vizazi vyenu vyote. Mafuta haya yasimiminiwe hata kidogo mutu yeyote wa kawaida, wala kusitengenezwe mafuta mengine ya aina hii. Haya ni mafuta matakatifu na yanapaswa kuwa siku zote matakatifu kwenu. Yeyote atakayetengeneza mafuta kama haya, au kumupakaa mutu asiyestahili kupakwa mafuta haya, mutu huyu atatengwa mbali na watu wake. Yawe akamwambia Musa: Utatwaa vipimo vinavyolingana vya viungo vitamu hivi: utomvu wa natafi, utomvu wa shekeleti, utomvu wa kelbena na ubani safi. Utatumia vitu hivyo kwa kutengeneza ubani kama vile unavyotengenezwa na fundi wa manukato, utiwe chumvi upate kuwa safi na mutakatifu. Kisha utasagwa na kufanya unga laini, upate kutumiwa ndani ya hema la mukutano na kulipakaa Sanduku la Agano, pahali nitakapokutana nawe. Huo utakuwa ubani mutakatifu kabisa kwenu. Musifanye hata kidogo ubani wa muchanganyiko huo kwa matumizi yenu wenyewe maana ubani huo utakuwa mutakatifu mbele yangu. Yeyote atakayejitengenezea ubani wa aina hiyo na kuutumia kama manukato yake pekee, atatengwa mbali na watu wake. Yawe akamwambia Musa: Mimi nimemuchagua Bezaleli mwana wa Uri mwana wa Huri, wa kabila la Yuda na kumujaza Roho wangu. Nimemupatia ufahamu na akili, maarifa na ufundi, kusudi afanye kazi za ufundi na kufanya kazi za kufua zahabu, feza na shaba. Nimemupatia ujuzi wa kuchonga mawe ya kupamba, kuchonga mbao, na ujuzi wa kila aina ya ufundi. Vilevile nimemuchagua Oholiabu mwana wa Ahisamaki wa kabila la Dani, afanye kazi pamoja naye. Vilevile nimewapa uwezo mukubwa watu wengine kwa ajili ya kazi mbalimbali, kusudi watengeneze vifaa vyote nilivyoagiza vifanywe: hema la mukutano, Sanduku la Agano na kiti cha ushuhuda juu yake, pamoja na vifaa vyake vyote, meza na vyombo vyake, kinara safi cha taa na vyombo vyake, mazabahu ya kufukizia ubani, mazabahu ya sadaka za kuteketezwa na vyombo vyake vyote, birika la maji pamoja na tako lake, nguo takatifu ya kuhani Haruni na wana wake ambao watafanya kazi ya ukuhani, mafuta ya kupakaa na ubani wenye harufu nzuri kwa ajili ya Pahali Patakatifu. Vitu hivyo vyote vitatengenezwa kulingana kabisa na jinsi nilivyokuamuru. Yawe akamwambia Musa: Uwaambie Waisraeli hivi: Ninyi mutashika hakika Sabato zangu, kwa sababu hizo ni kitambulisho kati yenu na mimi kwa vizazi vyote kwamba mimi ndimi ninayewatakasa. Mutashika Sabato, nayo itakuwa kwenu siku takatifu. Yeyote atakayeichafua siku hiyo anapaswa kuuawa. Na mutu atakayefanya kazi yoyote siku hiyo atatengwa mbali na watu wake. Mutafanya kazi zenu kwa muda wa siku sita, lakini siku ya saba ni siku ya Sabato, ni siku ya kupumzika ambayo ni takatifu kwa ajili ya Yawe. Mutu yeyote atakayefanya kazi yoyote siku hiyo lazima atauawa. Kwa hiyo Waisraeli watashika Sabato katika vizazi vyao vyote kama vile kitambulisho cha agano la milele. Jambo hili litakuwa kitambulisho cha kudumu kati ya Waisraeli na mimi, maana mimi Yawe nilifanya mbingu na dunia kwa muda wa siku sita, lakini siku ya saba niliacha kufanya kazi, nikapumzika. Yawe alipomaliza kuongea na Musa juu ya mulima Sinai, akamupatia Musa vile vibao viwili vya mawe ambavyo juu yake Mungu aliziandika zile amri kwa kidole chake mwenyewe. Watu walipoona kwamba Musa amechelewa kurudi kutoka juu ya mulima, wakakusanyika mbele ya Haruni na kumwambia: Basi! Ututengenezee miungu itakayotuongoza, maana hatujui jambo lililomupata yule Musa aliyetutoa katika inchi ya Misri. Haruni akawajibu: Mutwae pete za zahabu za masikio ya wake zenu, wana wenu na wabinti zenu, muniletee. Basi, watu wote wakatoa pete zote za zahabu za masikio yao, wakamuletea Haruni. Naye akazitwaa akaziyeyusha, akatengeneza sanamu ya mwana-ngombe. Watu wakapaaza sauti wakasema: Ee Israeli, huyu ndiye mungu wetu aliyetutoa katika inchi ya Misri. Kisha Haruni akamujengea yule mwana-ngombe mazabahu, halafu akatangaza: Kesho kutakuwa sikukuu kwa ajili ya Yawe. Kesho yake watu wakaamuka mapema wakatoa sadaka za kuteketezwa na sadaka za amani. Watu wakaikaa chini kwa kula na kunywa, kisha wakasimama na kucheza. Yawe akamwambia Musa: Teremuka chini kwa maana watu wako uliowaleta kutoka inchi ya Misri wamejipotosha wenyewe. Wameacha mara moja njia niliyowaamuru, wakajifanyia sanamu ya mwana-ngombe, nao wamemwabudu na kumutolea sadaka wakisema: Ee Israeli, huyu ndiye mungu wetu aliyetutoa katika inchi ya Misri! Ninawafahamu watu hawa. Wao wana vichwa vigumu. Sasa, usijaribu kunizuia. Uniache niwaangamize kwa kasirani kali. Kisha kutokana nawe nitaunda taifa kubwa. Lakini Musa akamusihi Yawe, Mungu wake, akisema: Ee Yawe, kwa nini hasira yako inawaka vikali juu ya watu wako uliowatoa katika inchi ya Misri kwa uwezo mukubwa na mukono wenye nguvu? Ukifanya hivyo, hakika Wamisri watasema: Aliwatoa kwa nia mbaya kwa kuwaua kwenye mulima na kuwateketeza kabisa katika dunia. Ee Yawe, tuliza hasira yako kali na kuacha jambo hilo baya ulilokusudia kufanya juu ya watu wako. Uwakumbuke watumishi wako, Abrahamu, Isaka na Israeli, ambao uliwaapia kwa nafsi yako mwenyewe, ukisema: Nitawazidisha wazao wenu kama nyota za mbinguni na inchi yote hii niliyowaahidia nitawapa vizazi vyenu wairizi milele. Basi, Yawe akaacha kuwafanyia watu wake lile jambo baya alilokuwa amesema. Kisha Musa akashuka kutoka juu ya mulima akiwa na vile vibao viwili vya agano katika mikono yake, vimeandikwa amri za Mungu pande zote. Vibao hivyo vilikuwa kazi ya Mungu mwenyewe na maandiko hayo Mungu mwenyewe aliyachora. Yoshua aliposikia kelele za watu, akamwambia Musa: Kuna kelele za vita ndani ya kambi. Lakini Musa akamujibu: Si kelele ya ushindi au kushindwa, lakini kelele ninayosikia ni kelele ya watu wanaoimba. Mara tu walipokaribia kambi walimwona yule mwana-ngombe na watu wakicheza. Hapo hasira ya Musa ikawaka kama moto, akatupa chini vile vibao kutoka mikono yake na kuvivunja pale chini ya mulima. Basi, akamutwaa yule mwana-ngombe akamuchoma kwa moto, akamusaga mpaka akakuwa unga, akakoroga unga huo katika maji na kuwalazimisha Waisraeli wakunywe. Musa akamwuliza Haruni: Walikufanya nini watu hawa hata ukawaingiza katika zambi kubwa hivyo? Haruni akamujibu: Ninakuomba, ee bwana wangu, hasira yako isiniwakie mimi mutumishi wako. Unafahamu jinsi watu hawa wanavyokuwa tayari kutenda maovu. Walikuja wakaniambia: Utufanyie miungu ambayo itatuongoza, maana yule Musa aliyetutoa katika inchi ya Misri hatujui jambo lililomupata. Nami nikawaambia, kila mumoja aliyekuwa na pete za zahabu azilete. Basi, wakaniletea, nami nikaziyeyusha juu ya moto na huyu mwana-ngombe akatokea. Basi, Musa alipoona kwamba watu wameasi na kufanya wanavyopenda (kwa kuwa Haruni aliwafanya waasi na kufanya wanavyopenda na kujiletea haya mbele ya waadui zao), Musa akasimama mbele ya mulango wa kambi na kuuliza: Ni nani anayekuwa upande wa Yawe? Akuje kwangu. Wana wote wa Lawi wakakusanyika pamoja mbele yake. Akawaambia: Yawe, Mungu wa Israeli, anasema hivi: Kila mutu ajifungie upanga wake kwenye kiuno, azunguke kila pahali katika kambi, kutoka mulango moja mpaka mwingine, na kila mumoja amwue ndugu yake, rafiki yake na jirani yake. Wana wa Lawi wakafanya kama vile Musa alivyowaagiza. Siku hiyo watu yapata elfu tatu waliuawa. Musa akasema: Leo mumejitakasa ninyi wenyewe kwa kumutumikia Yawe, kwa vile hamukusita hata kuwaua watoto wenu au wandugu zenu. Mungu awajalie baraka leo hii. Kesho yake Musa akawaambia watu: Mumetenda zambi kubwa! Sasa nitamwendea Yawe juu kwenye mulima; labda nitafanya upatanisho kwa ajili ya zambi yenu. Hivyo Musa akarudi kwa Yawe, akamwambia: Ninasikitika! Watu hawa wametenda zambi kubwa. Wamejifanyia wenyewe miungu ya zahabu. Lakini sasa, ninakuomba uwasamehe zambi yao. Ikiwa hautawasamehe, ninakusihi unifute mimi katika kitabu chako ambamo uliwaandika watu wako. Lakini Yawe akamwambia Musa: Nitamufuta katika kitabu changu mutu yeyote aliyenitendea zambi. Lakini sasa kwenda uwaongoze watu mpaka pahali nilipokuambia. Malaika wangu atakutangulia. Hata hivyo, siku nitakapowafikia, nitawaazibu kwa sababu ya zambi yao. Yawe akawaletea watu ugonjwa mukali, kwa kuwa walimwomba Haruni awafanyie yule mwana-ngombe wa zahabu. Yawe akamwambia Musa: Anza safari uondoke hapa, wewe na watu hao uliowatoa katika inchi ya Misri. Muende katika inchi niliyowapia Abrahamu, Isaka na Yakobo, nikisema: Nitawapa wazao wenu inchi hii. Nitamutuma malaika awaongoze. Nitawafukuza Wakanana, Waamori, Wahiti, Waperizi, Wahivi na Wayebusi. Muende katika inchi hiyo inayotiririka maziwa na asali. Lakini kwa sababu ninyi ni wenye vichwa vigumu sitakwenda pamoja nanyi, nisiwaangamize katika njia. Watu wakalia waliposikia habari hizi mbaya, wala hakuna aliyevaa mapambo yake. Walifanya hivyo maana Yawe alikuwa amemwambia Musa: Uwaambie Waisraeli: Ninyi ni watu wenye vichwa vigumu. Nikienda pamoja nanyi kwa muda mufupi tu, nitawaangamiza. Hivyo muvue mapambo yenu kusudi nijue namna ya kuwatendea. Basi, Waisraeli wakavua mapambo yao tangu walipoondoka kwenye mulima Horebu. Musa alikuwa na desturi ya kuchukua lile hema na kulisimika inje ya kambi. Hema hilo alilipa jina, hema la mukutano. Mutu yeyote aliyetaka shauri kwa Yawe alikwenda kwenye hema la mukutano inje ya kambi. Kila mara Musa alipotoka kwenda kwenye hema hilo, kila mutu alisimama kwenye mulango wa hema yake na kumwangalia Musa mpaka alipoingia ndani ya hilo hema. Wakati Musa alipoingia ndani ya hilo hema, munara wa wingu ulitua kwenye mulango wa hema, na Yawe akaongea naye. Watu wote walipouona ule munara wa wingu umesimama kwenye mulango wa hema, kila mumoja wao alisimama na kuabudu kwenye mulango wa hema lake. Hivi ndivyo Yawe alivyokuwa akiongea na Musa uso kwa uso, kama mutu na rafiki yake. Kisha Musa alirudi tena katika kambi. Naye kijana Yoshua mwana wa Nuni ambaye alikuwa mutumishi wake hakuondoka ndani ya hema. Musa akamwambia Yawe: Wewe unaniambia: Uwaongoze watu hawa, lakini haujanijulisha ni nani utakayemutuma anisaidie. Hata hivyo umesema kwamba unanijua kwa jina langu na vilevile kwamba nimepata kukubaliwa mbele yako. Sasa basi, ninakusihi, kama nimepata kukubaliwa mbele yako, unionyeshe sasa njia zako, kusudi nipate kukujua na kupata kukubaliwa mbele yako. Ninaomba ukumbuke vilevile kwamba taifa hili ni watu wako. Mungu akasema: Mimi mwenyewe nitakwenda pamoja nawe na nitakupa raha. Musa akasema: Kama wewe peke yako hautakwenda pamoja nami, basi, usituondoe pahali hapa. Maana namna gani itajulikana kwamba nimepata kukubaliwa mbele yako, mimi na watu wako kama usipokwenda pamoja nasi? Ukienda pamoja nasi itatufanya mimi na watu wako kuwa watu wa pekee kati ya watu wote katika dunia. Yawe akamwambia Musa: Kwa sababu umepata kukubaliwa mbele yangu, nami ninakujua kwa jina lako, jambo hilihili ulilolisema nitalifanya. Musa akasema: Ninakusihi unionyeshe utukufu wako. Yawe akamujibu: Nitapita mbele yako na kukuonyesha uzuri wangu wote nikilitangaza jina langu, Yawe. Mimi nitamuhurumia yule ninayependa kumuhurumia; nitamurehemu yule ninayependa kumurehemu. Lakini hautaweza kuniona uso maana hakuna mwanadamu yeyote atakayeniona na kuishi. Kisha Yawe akamwambia Musa: Kuna pahali karibu nami ambapo utasimama juu ya jiwe. Utukufu wangu utakapokuwa unapita, nitakutia katika pango chini ya jiwe na kukufunika kwa mukono wangu, mpaka nitakapokuwa nimepita. Halafu nitaondoa mukono wangu nawe utaona mugongo wangu, lakini uso wangu hautauona. Yawe akamwambia Musa: Chonga vibao viwili vya mawe kama vile vya kwanza, nami nitaandika maneno yale yaliyokuwa katika vile vibao vya kwanza ulivyovunja. Ukuwe tayari kesho asubui, ukuje kukutana nami juu ya mulima Sinai. Mutu yeyote asikuje pamoja nawe, wala asionekane popote kwenye mulima, wala kondoo au ngombe wasikulishwe karibu yake. Basi, Musa akachonga vibao viwili vya mawe kama vile vya kwanza. Akaondoka asubui mapema, akapanda juu ya mulima Sinai, kama vile Yawe alivyomwamuru, akiwa na vile vibao viwili vya mawe katika mikono yake. Yawe akashuka katika wingu, akasimama pamoja na Musa, akataja jina lake: Yawe. Kisha Yawe akapita mbele ya Musa akitangaza tena: Yawe, Yawe, ni Mungu mwenye rehema na huruma, si mwepesi wa hasira, ni mwingi wa wema na uaminifu. Anawatendea mema maelfu, anawasamehe uovu, makosa na zambi. Lakini hataacha kumwazibu mwenye kosa. Anawalipiza watoto na wajukuu uovu wa baba na babu zao, hata kizazi cha tatu na cha ine. Musa akainama uso mpaka chini haraka, akamwabudu Mungu. Kisha akasema: Ee Bwana wangu, kama nimepata kukubaliwa mbele yako, ninakuomba uende pamoja nasi. Watu hawa ni wenye vichwa vigumu, lakini utusamehe uovu wetu na zambi yetu, utupokee kama watu wako mwenyewe. Yawe akamwambia Musa: Sasa ninafanya agano na watu wako. Nitatenda maajabu mbele yao ambayo hayajapata kutendwa katika dunia yote, wala katika taifa lolote. Na watu wote munaoishi kati yao wataona matendo yangu makubwa. Maana nitafanya jambo la ajabu kwa ajili yako. Mushike amri ninazowapa leo. Nitawafukuza mbele yenu Waamori, Wakanana, Wahiti, Waperizi, Wahivi na Wayebusi. Mufanye angalisho musifanye agano na wakaaji wa inchi munayoiendea, maana hiyo itakuwa mutego kati yenu. Lakini mutabomoa mazabahu zao na kuvunja nguzo zao za ibada na sanamu zao za Ashera. Musiabudu mungu yeyote mwingine, maana mimi Yawe ninajulikana kwa jina: Mwenye Wivu. Mimi ni Mungu mwenye wivu. Musifanye mapatano yoyote na wakaaji wa inchi hiyo, maana watakapoabudu miungu yao ya uongo na kuitambikia, watawaalika, nanyi mutashawishiwa kula vyakula wanavyotambikia miungu yao. Vijana wenu wakioa wabinti zao, na hao wabinti wanaoabudu miungu yao, watawashawishi vijana wenu kufuata miungu yao. Musijifanyie miungu ya uongo ya chuma. Mutashika sikukuu ya Mikate Isiyotiwa Chachu. Kwa muda wa siku saba mutakula mikate isiyotiwa chachu wakati uliopangwa katika mwezi wa Abibu, kama vile nilivyowaamuru, kwa sababu katika mwezi huo wa Abibu mulitoka Misri. Kila muzaliwa wa kwanza mwanaume ni wangu, pamoja na wazaliwa wa kwanza dume wa nyama wako wote, wa ngombe na wa kondoo. Muzaliwa wa kwanza wa punda utamukomboa kwa kunitolea kondoo. Kama hautamukomboa utamuvunja shingo. Watoto wenu wote wanaume ambao ni wazaliwa wa kwanza mutawakomboa. Mutu yeyote asikuje mbele yangu mikono mitupu. Siku sita mutafanya kazi, lakini siku ya saba mutapumzika, hata ikiwa ni wakati wa kulima au kuvuna. Mutashika sikukuu ya majuma kwa mwanzo wa wakati wa mavuno ya ngano na kufanya sikukuu ya kukusanya mavuno kwa mwisho wa mwaka. Mara tatu kwa mwaka wanaume wote watakusanyika mbele ya Bwana wenu, Yawe, Mungu wa Israeli. Nitafukuza mataifa mengine mbele yenu na kupanua mipaka yenu. Hakuna mutu yeyote atakayetamani inchi yenu wakati munapokusanyika kwa kuniabudu, mimi Yawe, Mungu wenu, mara tatu kila mwaka. Musinitolee damu ya sadaka yangu pamoja na chachu, wala sadaka ya sikukuu ya Pasaka isiachwe mpaka asubui. Mazao ya kwanza ya shamba yako utayaleta katika nyumba yangu mimi Yawe, Mungu wako. Usipike mwana-kondoo au mwana-mbuzi katika maziwa ya mama yake. Yawe akamwambia Musa: Andika maneno haya, maana kulingana na maneno haya, ninafanya agano nawe na watu wa Israeli. Musa alikaa kule kwenye mulima pamoja na Yawe siku makumi ine, muchana na usiku. Hakukula chakula wala kunywa maji. Aliandika maneno yote ya agano na zile amri kumi. Musa alipokuwa anashuka toka kwenye mulima Sinai akiwa na vile vibao viwili vyenye maneno ya agano katika mikono yake, hakujua kwamba uso wake ulikuwa unangaa kwa sababu alikuwa ameongea na Yawe. Haruni na watu Waisraeli wote walipomwona wakaogopa kumukaribia, maana uso wake ulikuwa unangaa. Lakini Musa alimwita Haruni na viongozi wote wa Waisraeli waende karibu naye, kisha akazungumuza nao. Kisha Waisraeli wote wakakuja karibu naye, naye akawapa amri zote ambazo Yawe alimupa kule juu ya mulima Sinai. Musa alipomaliza kuzungumuza na watu akaufunika uso wake kwa kitambaa. Lakini ikakuwa kwamba kila mara Musa alipokwenda kuongea na Yawe katika hema la mukutano, aliondoa kile kitambaa mpaka alipotoka inje. Na alipotoka inje aliwaambia Waisraeli mambo yote aliyoamuriwa, nao Waisraeli waliona uso wake unangaa. Halafu Musa alifunika tena uso wake kwa kitambaa mpaka alipokwenda kuongea na Yawe. Musa akakusanya Waisraeli wote pamoja, akawaambia: Haya ndiyo mambo ambayo Yawe amewaamuru kufanya: Kwa siku sita mutafanya kazi zenu. Lakini siku ya saba ni Sabato, siku ya mapumziko ambayo ni takatifu kwa Yawe. Yeyote atakayefanya kazi siku hiyo lazima auawe. Musiwashe hata moto katika makao yenu siku ya Sabato. Musa akawaambia Waisraeli wote: Hili ndilo jambo ambalo Yawe amewaamuru kufanya: Mutatoa katika mali zenu muchango wa kumupa Yawe. Kila mutu mwenye moyo mwema atamuletea Yawe muchango: sadaka, feza, shaba; sufu ya samawi, ya zambarau na nyekundu; kitani safi iliyosokotwa; manyoya ya mbuzi; ngozi za kondoo dume zilizotiwa rangi nyekundu, ngozi za mbuzi; mbao za mujohoro, mafuta kwa ajili ya taa, viungo kwa ajili ya mafuta ya kupakaa na kwa ajili ya ubani wenye harufu nzuri; mawe vya sardoniki na mawe mengine kwa ajili ya mapambo ya kizibao na kifuko cha kifua. Kila mutu mwenye ujuzi wa kazi fulani kati yenu atakuja kufanya vitu vyote Yawe alivyoamuru: kutengeneza hema takatifu, kifuniko chake na pazia lake, vifungio vyake, miti yake, vikalio vyake; Sanduku la Agano pamoja na miti yake, kiti cha rehema, pazia la Pahali Patakatifu Sana; meza na miti yake pamoja na vyombo vyake vyote, mikate iliyotolewa kwa Yawe; vinara vya taa pamoja na vyombo vyake vyote, taa zake na mafuta yake; mazabahu ya ubani na miti yake, mafuta ya kupakaa na ubani wenye harufu nzuri, pazia la mulango wa hema takatifu; mazabahu ya sadaka za kuteketezwa pamoja na wavu wa shaba, miti yake pamoja na vyombo vyake vyote, birika na tako lake; nguo za kiwanja, nguzo zake na vikalio vyake, pazia la mulango wa kiwanja; misumari ya hema takatifu na ya kiwanja pamoja na kamba zake; nguo zilizofumwa vizuri kabisa kwa ajili ya kazi ya Pahali Patakatifu, ni kusema nguo takatifu ya kuhani Haruni na ya wana wake, kwa ajili ya kazi yao ya ukuhani. Basi, Waisraeli wakaondoka mbele ya Musa. Kila mutu aliyevutwa na kusukumwa ndani ya moyo wake alimutolea Mungu muchango wake kwa ajili ya hema la mukutano, kazi zake zote na nguo yake takatifu. Hivyo wote wenye moyo safi, wanaume na wanawake, wakaleta pete za masikio na za muhuri, vikuku na kila aina ya mapambo ya zahabu. Kila mutu akamutolea Yawe kitu cha zahabu. Kila mutu alileta kitu chochote alichokuwa nacho kama vile sufu ya rangi ya samawi, zambarau na nyekundu, au kitani safi, au manyoya ya mbuzi au ngozi ya kondoo iliyotiwa rangi nyekundu. Kila mutu aliyeweza kutoa feza au shaba aliileta kwa Yawe kama matoleo yake. Tena mutu yeyote aliyekuwa na mbao za mujohoro alileta vilevile. Wanawake wote waliokuwa na ujuzi wa kufuma walileta vitu walivyofuma kwa sufu ya rangi ya samawi, zambarau na nyekundu na kitani safi iliyosokotwa. Na wanawake wote waliokuwa na ujuzi walisokota manyoya ya mbuzi. Viongozi walileta mawe ya rangi na mawe mengine kwa ajili ya kizibao na kifuko cha kifua. Walileta vilevile viungo na mafuta kwa ajili ya taa, mafuta ya kupakaa na ubani wenye harufu nzuri. Waisraeli wote, wanaume na wanawake, ambao walivutwa ndani ya moyo wao kuleta kitu chochote kwa ajili ya kazi ambayo Yawe alikuwa amemwagiza Musa ifanyike, walileta vitu hivyo kwa mapenzi yao, kama vile muchango wa kumupa Yawe. Musa akawaambia Waisraeli: Muangalie! Yawe amemuchagua Bezaleli mwana wa Uri mwana wa Huri, wa kabila la Yuda. Amemujaza Roho wake, amemupa ujuzi, akili, maarifa na ufundi, afanye michoro ya ufundi na kufanya kazi za kufua zahabu, feza na shaba; achonge mawe ya kupamba na mbao kwa ajili ya kazi zingine zote za kifundi. Vilevile amemwongoza yeye na Oholiabu mwana wa Ahisamaki, wa kabila la Dani wawafundishe wengine. Amewapa ujuzi wa kufanya kila kazi ya ufundi au inayofanywa na watu wa akili au wafundi wa kushona kwa sufu ya rangi ya samawi, ya zambarau, nyekundu na kitani safi iliyosokotwa kwa kutumia ufundi wowote wa akili. Bezaleli na Oholiabu, pamoja na kila mwanaume ambaye Yawe amemujalia uwezo na akili ya kujua namna ya kufanya kazi zote katika majengo ya hema takatifu, atafanya kazi kulingana na yote ambayo Yawe aliamuru. Musa akamwita Bezaleli na Oholiabu na kila mutu ambaye alikuwa amejaliwa ujuzi na Yawe na kila mutu ambaye moyo wake ulimusukuma kufanya kazi kwa nia nzuri. Hao wakapokea kutoka kwa Musa vitu vyote vilivyotolewa na Waisraeli kwa mapenzi yao kwa ajili ya kazi ya hema takatifu. Watu waliendelea kumuletea michango yao kufuatana na mapenzi yao kila asubui. Watu wote wenye ujuzi waliokuwa wanafanya kazi za kila namna za kujenga hema la mukutano walitoka, kila mumoja katika kazi yake, wakamwendea Musa na kumwambia: Watu wameleta vitu vingi zaidi ya vile vinavyohitajiwa kwa kazi Yawe aliyotuagiza tufanye. Basi, Musa akaagiza: Mutu yeyote, akuwe mwanaume au mwanamuke, asilete muchango zaidi kwa ajili ya hema takatifu. Watu wakazuiwa kuleta vitu, maana vile walivyokuwa wameleta vilitosha kwa kazi hiyo na kubaki. Wanaume wote wenye ujuzi wakatengeneza hema takatifu kwa mapazia kumi ya kitani safi iliyosokotwa, na kwa sufu ya rangi ya samawi, zambarau na nyekundu, na kuchora makerubi. Urefu wa kila pazia ulikuwa metre kumi na mbili na upana metre mbili. Mapazia yote yalikuwa ya kipimo kimoja. Aliyaunga mapazia matano kufanya kipande kimoja na kufanya vile vile na yale mengine matano. Alitengeneza kamba za rangi ya samawi kwenye upindo wa pazia la mwisho la kipande cha kwanza na kamba zingine katika pazia la mwisho la kipande cha pili. Alitia kamba makuni tano katika pazia la kwanza la kipande cha kwanza na kamba makuni tano kwenye utepe wa pazia la pili. Kamba zote zilielekeana. Kisha akatengeneza vifungio makuni tano vya zahabu kwa kuunganishia vile vipande viwili vya mapazia, hivyo hema likakuwa kitu kimoja. Kisha alitengeneza vilevile kifuniko cha hema kwa mapazia kumi na moja ya manyoya ya mbuzi. Kila pazia lilikuwa na urefu wa metre kumi na tatu na upana wa metre mbili. Mapazia yote kumi na moja yalikuwa ya kipimo kilekile. Basi, akaunganisha mapazia matano pamoja na mapazia sita pamoja. Kisha akafanya kamba makuni tano kwenye upindo wa pazia la mwisho la kipande cha kwanza na kamba makuni tano kwenye upindo wa kipande cha pili. Halafu akatengeneza vifungio makuni tano vya shaba kwa kuunganishia vile vipande viwili vya mapazia na hivyo kufanya pazia moja la hema. Kisha akatengeneza kifuniko cha ngozi laini ya kondoo dume na juu yake kifuniko kingine cha ngozi laini ya mbuzi. Halafu akatengenezea hema mbao za mujohoro za kusimama wima. Kila ubao ulikuwa na urefu wa metre ine na upana wa sentimetre makumi sita na sita. Kila ubao ulikuwa na ndimi mbili za kuunganishia. Mbao zote za hema alizifanyia ndimi. Mbao hizo za hema zilitengenezwa hivi: mbao makumi mbili upande wa kusini, na vikalio makumi ine vya feza chini ya hizo mbao makumi mbili, vikalio viwili chini ya kila ubao kwa kushikilia zile ndimi zake mbili. Na upande wa pili, ni kusema upande wa kaskazini wa hema, alitengeneza vilevile mbao makumi mbili, na vikalio vyake makumi ine vya feza; vikalio viwili chini ya kila ubao. Upande wa nyuma, ni kusema upande wa magaribi wa hema, alitengeneza mbao sita. Alitengeneza vilevile mbao mbili kwa ajili ya pembe za hema upande wake wa nyuma. Mbao hizo mbili za pembeni ziliachana chini lakini zilishikamanishwa kwenye pete ya kwanza. Mbao mbili kwa ajili ya hizo pembe mbili zilitengenezwa namna hiyo. Hivyo kulikuwa mbao nane na vikalio vyake vya feza kumi na sita, vikalio viwili chini ya kila ubao. Alitengeneza vilevile miti ya mujohoro: miti tano kwa ajili ya mbao za upande mumoja wa hema, miti tano kwa ajili ya upande wa pili wa hema, na miti tano kwa ajili ya mbao za upande wa nyuma wa hema uliokuwa upande wa magaribi. Alitengeneza muti wa katikati uliofika nusu ya jengo la hema ambao ulipenya katikati kutoka mwisho mpaka mwisho. Mbao zote alizipakaa zahabu, akatengeneza na pete za zahabu za kushikilia miti ile ambayo vilevile aliipakaa zahabu. Alitengeneza pazia la nyuzi za rangi ya samawi, zambarau na nyekundu na kitani safi iliyosokotwa. Pazia hilo lilipambwa na makerubi kwa ufundi. Alitengeneza nguzo ine za mujohoro, akazipakaa zahabu na kuzitilia vifungio vya zahabu. Vilevile alizifanyia vikalio vine vya feza. Vilevile, kwa ajili ya mulango wa hema, alitengeneza pazia kwa nyuzi za rangi ya samawi, zambarau na nyekundu, na kitani safi iliyosokotwa, nalo pazia lilipambwa vizuri, na nguzo zake tano zikiwa na vifungio. Chongo zake na vyuma vyake alivipakaa zahabu, lakini vikalio vyake vitano vilikuwa vya shaba. Bezaleli akatengeneza sanduku kwa mbao za mujohoro. Urefu wake ulikuwa sentimetre mia moja na kumi, upana sentimetre makumi sita na sita, na urefu kwenda juu sentimetre makumi sita na sita. Akalipakaa zahabu safi ndani na inje na kulifanyia ukingo wa zahabu pande zote. Kisha akatengeneza pete ine za zahabu za kulibebea, akazitia kwenye pembe zake, kila pembe pete moja. Akatengeneza miti ya mujohoro na kuipakaa zahabu. Miti hiyo akaipitisha katika zile pete zinazokuwa katika pande mbili za sanduku, kwa ajili ya kulibebea. Akatengeneza kiti cha rehema cha zahabu safi; urefu wake sentimetre mia moja na kumi na upana wake sentimetre makumi sita na sita. Akatengeneza vilevile makerubi wawili kwa kufua zahabu kwenye miisho ya kifuniko hicho; kerubi mumoja mwisho huu na mwingine mwisho mwingine. Akatengeneza makerubi wale kwenye miisho ya kifuniko hicho, wakikuwa kitu kimoja na kifuniko. Makerubi wale walikuwa wakielekeana, mabawa yao yakikunjuliwa na kukifunika kifuniko cha sanduku, nyuso zao zilikielekea kifuniko cha sanduku. Vilevile akatengeneza meza ya mujohoro yenye urefu wa sentimetre makumi nane na nane, upana sentimetre makumi ine na ine, na urefu kwenda juu sentimetre makumi sita na sita. Akapakaa zahabu safi na kuitengenezea ukingo wa zahabu. Akaizungushia ubao wenye upana wa milimetre makumi saba na tano, na kuifanyia ukingo wa zahabu. Akaitengenezea pete ine za zahabu na kuzitia katika pembe zake ine pahali miguu ilipoishia. Pete hizo za kushikilia ile miti ya kuibebea ziliwekwa karibu na ule muzunguko wa ubao. Akatengeneza miti miwili ya mujohoro ya kuibebea, akaipakaa zahabu. Akatengeneza vyombo vya zahabu safi vya kuweka juu ya meza: sahani zake na visahani kwa ajili ya ubani, na bilauri zake na bakuli kwa ajili ya sadaka za kinywaji. Akatengeneza vilevile kinara cha taa kwa zahabu safi. Tako lake na muti wa hicho kinara ulikuwa kitu kimoja pamoja na vikombe vyake, vifundo vyake na maua yake. Matawi sita yalitokeza kila upande wa muti wake, matawi matatu upande mumoja na matawi matatu upande mwingine. Katika kila tawi kulikuwa vikombe vitatu mufano wa maua ya lozi, kila kimoja na kifundo chake na ua lake. Na katika muti kulikuwa vikombe vine mufano wa maua ya lozi, pamoja na vifundo vyake na maua yake. Kulikuwa kifundo kila pahali matawi mawilimawili yalipotokea kufuatana na yale matawi sita yanayotoka kwa kile kinara. Vifundo hivyo na matawi vilikuwa kitu kimoja na kinara hicho na chote kilifuliwa kwa zahabu safi. Akatengeneza taa zake saba, koleo zake na visahani vyake kwa zahabu safi. Akatengeneza kinara hicho na vifaa vyake kwa kilo makumi tatu na tano za zahabu. Akatengeneza mazabahu ya kufukizia ubani kwa mbao za mujohoro. Mazabahu hiyo ilikuwa ya muraba, sentimetre makumi ine na tano kwa sentimetre makumi ine na tano, na urefu kwenda juu sentimetre makumi tisa. Pembe za mazabahu hiyo zilikuwa kitu kimoja na mazabahu yenyewe. Yote aliipakaa zahabu safi: upande wake wa juu, pande zake za ubavu na pembe zake. Vilevile akaitengenezea ukingo wa zahabu. Akatengeneza pete mbili za zahabu chini ya ukingo kwenye pande mbili zinazoelekeana. Pete hizo zilitumika kushikilia miti ya kuibebea. Akafanya miti miwili ya mujohoro na kuipakaa zahabu. Akatengeneza mafuta matakatifu ya kupakaa na ubani safi wenye harufu nzuri uliochanganywa vizuri kama manukato. Akatengeneza mazabahu kwa ajili ya sadaka za kuteketezwa kwa moto. Mazabahu hiyo ilikuwa ya muraba, metre mbili na sentimetre makumi mbili kwa metre mbili na sentimetre makumi mbili, na urefu kwenda juu metre moja na sentimetre makumi mbili. Katika kila pembe ya mazabahu hiyo akatengeneza upembe uliokuwa umeundwa kutokana na mazabahu yenyewe. Mazabahu hiyo yote akaipakaa shaba. Akatengeneza vilevile vyombo vyote kwa ajili ya mazabahu: vyungu, majembe, mabeseni, kanya na visahani vya kutwalia moto. Vyombo vyake vyote akavitengeneza kwa shaba. Akatengeneza wavu wa shaba, akautia chini ya ukingo wa mazabahu mpaka katikati ya mazabahu. Katika pembe ine akatengeneza pete ine za kubebea hiyo mazabahu. Akatengeneza miti ya mujohoro na kuipakaa shaba. Akaitia ile miti katika zile pete zilizokuwa kando ya mazabahu kwa kuibebea. Mazabahu hiyo iliyotengenezwa kwa mbao ilikuwa wazi ndani. Kisha akatengeneza birika la shaba na tako lake la shaba. Birika hilo lilitengenezwa kwa kutumia vioo vya shaba vya wanawake waliotumika kwenye mulango wa hema la mukutano. Kisha akatengenezea hema upango. Mapazia ya upande wa kusini wa upango yalikuwa ya kitani safi iliyosokotwa na yenye urefu wa metre makumi ine na ine; nayo yalishikiliwa na nguzo makumi mbili za shaba zenye vikalio makumi mbili vya shaba. Lakini vifungio vya nguzo hizo na kamba zake vilikuwa vya feza. Upande wa kaskazini urefu wa pazia ulikuwa metre makumi ine na ine, na nguzo zake makumi mbili za shaba, lakini vifungio vya nguzo hizo na kamba zake vilikuwa vya feza. Upande wa magaribi ulikuwa na pazia yenye urefu wa metre makumi mbili na mbili, nguzo zake kumi na vikalio vyake kumi. Vifungio vya nguzo na kamba zake vilikuwa vya feza. Upande wa mashariki, kulikuwa mulango, uliokuwa na upana wa metre makumi mbili na mbili. Pazia la kila upande wa mulango lilikuwa na upana wa metre sita na nusu, pamoja na nguzo tatu na vikalio vyake vitatu. Upande mwingine vilevile ulikuwa na pazia yenye upana wa metre sita na nusu, pamoja na nguzo tatu na vikalio vyake vitatu. Mapazia yote kuzunguka upango yalikuwa ya kitani safi iliyosokotwa. Vikalio vyote vya nguzo vilikuwa vya shaba, lakini vifungio vya nguzo hizo na kamba zake vilikuwa vya feza. Vifungio vyake vilikuwa vya feza; vilevile nguzo zake zote zilishikamanishwa kwa fito za feza. Pazia la mulango wa upango lilitengenezwa kwa sufu ya rangi ya samawi, zambarau na nyekundu, na kitani safi iliyosokotwa, na kupambwa vizuri. Nalo lilikuwa na urefu wa metre tisa na urefu kwenda juu metre mbili, kulingana na mapazia ya upango. Vilevile nguzo zake zilikuwa ine na vikalio vine vya shaba. Vifungio vyake vilikuwa vya feza, hata nguzo zake na kamba zake vilikuwa vya feza. Misumari yote ya hema na ya upango kandokando ya hema vilikuwa vya shaba. Hii ndiyo hesabu ya vifaa vilivyotumika katika kujenga hema la kuchunga vile vibao vya agano. Hesabu hii ilitayarishwa na Walawi kwa amri ya Musa, chini ya uongozi wa Itamari mwana wa kuhani Haruni. Bezaleli mwana wa Uri mwana wa Huri, wa kabila la Yuda, alifanya kila kitu ambacho Yawe alimwamuru Musa. Alisaidiwa na Oholiabu mwana wa Ahisamaki, wa kabila la Dani, fundi mukubwa wa kutia mapambo, kufanya michoro na kupamba kwa nyuzi za sufu ya rangi ya samawi, zambarau na nyekundu na kitani safi iliyosokotwa. Zahabu yote waliyomutolea Yawe kwa ajili ya kujenga hema takatifu ilikuwa na uzito wa kilo mia nane makumi saba na saba na grama mia tatu kulingana na vipimo vya hema takatifu. Feza waliyochanga hao waliohesabiwa ilikuwa ya uzito wa kilo elfu tatu kumi na saba na grama mia saba makuni tano kulingana na vipimo vya hema takatifu. Kila mutu aliyehesabiwa tangu umri wa miaka makumi mbili na moja na zaidi alitoa muchango wake wa feza grama tano. Wanaume wote waliohesabiwa walikuwa elfu mia sita na tatu na mia tano na makuni tano. Kilo elfu tatu za feza zilitumika kwa kutengeneza vile vikalio mia moja vya hema takatifu na lile pazia, ni kusema kilo makumi tatu kwa kila kikalio. Zile kilo kumi na saba na grama makumi saba na tano zilizobakia, zilitumika kwa kutengeneza vifungio vya nguzo na kuvipakaa vichwa vya nguzo na kutengeneza kamba. Jumla ya muchango wa shaba Waisraeli waliomutolea Yawe ilikuwa na uzito wa kilo elfu mbili mia moja makumi mbili na ine. Bezaleli akatumia shaba hiyo kwa kutengeneza vikalio vya mulango wa hema la mukutano, mazabahu ya shaba pamoja na wavu wake wa shaba, vyombo vyote vya mazabahu, vikalio vya upango uliolizunguka hema la mukutano na vya mulango wa upango na misumari yote ya hema takatifu na ya upango. Kwa kutumia sufu ya rangi ya samawi, zambarau na nyekundu walifuma nguo za kuvaa wakati wa kutumika katika Pahali Patakatifu. Walimushonea Haruni nguo takatifu kama vile Yawe alivyomwamuru Musa. Wakatengeneza kizibao kwa nyuzi za zahabu, kwa sufu ya rangi ya samawi, zambarau na nyekundu, na kwa kitani safi iliyosokotwa. Wakafua zahabu na kuikata katika nyuzi nyembamba kwa kuzifuma pamoja na sufu ya rangi ya samawi, ya zambarau na nyekundu, na kitani safi iliyosokotwa kwa ufundi. Kizibao hicho kilivaliwa kwa kamba mbili juu ya mabega zilizoshonewa kwenye incha zake mbili. Mukaba uliofumwa kwa ufundi juu yake kwa kuifunga ulikuwa kitu kimoja na kizibao hicho, na ulitengenezwa kwa vitu hivyohivyo: zahabu, sufu ya samawi, zambarau na nyekundu, na kitani safi iliyosokotwa, kama vile Yawe alivyomwamuru Musa. Kisha wakatayarisha mawe ya sardoniki na kuyapanga katika kingo za zahabu. Nayo yalichorwa, kama vile mutu anavyochora muhuri, majina kumi na mawili ya wana wa Israeli. Wakaweka mawe yale juu ya mikaba ya mabega za kila kizibao kuwa ukumbusho wa makabila kumi na mawili ya Israeli, kama vile Yawe alivyomwamuru Musa. Wafundi walitengeneza kifuko cha kifua kama vile walivyotengeneza kile kizibao, kwa zahabu, kwa sufu ya rangi ya samawi, ya zambarau na ya nyekundu, na kwa kitani safi iliyosokotwa. Kifuko hicho kilikuwa cha muraba, sentimetre makumi mbili na mbili kwa sentimetre makumi mbili na mbili nacho kilikunjwa. Kifuko hicho kilipambwa kwa mistari mine ya mawe ya bei kali. Mustari wa kwanza ulikuwa wa akiki, topazi na almasi nyekundu. Mustari wa pili ulikuwa wa zumaridi, yakuti-samawi na almasi. Mustari wa tatu ulikuwa wa yasinto, akiki nyekundu na ametisto. Mustari wa ine ulikuwa wa zabarajadi, shohamu na yaspi. Yote yalifungwa ndani ya kingo za zahabu. Basi, kulikuwa mawe kumi na mawili yaliyochorwa juu yake majina kumi na mawili ya wana wa Israeli. Yalikuwa yamechorwa kama vile wanavyochora muhuri, juu ya kila moja kulichorwa jina kwa ukumbusho wa makabila kumi na mawili. Walitengenezea kile kifuko cha kifua mikufu ya zahabu safi. Wakatengeneza kingo mbili za zahabu safi na pete mbili za zahabu, na kutia pete hizo kwenye incha mbili za juu za kifuko hicho. Mikufu hiyo miwili ya zahabu wakaifunga kwenye pete hizo za kifuko cha kifua. Zile incha mbili za mikufu ya zahabu wakazitia kwenye zile kingo mbili wakazishikamanisha na vile vipande viwili vya mabega vya kizibao, upande wa mbele. Wakatengeneza pete mbili za zahabu, wakazitia kwenye incha mbili za chini upande wa ndani wa kifuko hicho cha kifua karibu na kizibao. Wakatengeneza pete zingine mbili za zahabu na kuzitia mbele katika incha za chini za vipande vya kizibao, pahali kinapoungana na ule mukaba uliofumwa kwa ufundi. Wakafunga kifuko cha kifua kwenye kizibao kwa kufunganisha pete zake na kizibao kwa kamba ya rangi ya samawi, kusudi kifuko hicho kisiregee lakini kiikalie ule mukaba uliofumwa kwa ufundi, kama vile Yawe alivyomwamuru Musa. Akatengeneza kanzu ya kuvaa ndani ya kizibao ya rangi ya samawi. Koti hilo lilikuwa na nafasi ya kupitishia kichwa katikati, nalo lilizungushiwa utepe uliofumwa kusudi isichanike. Kwenye upindo wa chini wa kanzu walifuma mapambo ya makomamanga ya rangi ya samawi, ya zambarau na nyekundu, na kitani safi iliyosokotwa. Kisha walitengeneza kengele za zahabu na kisha kila komamanga walitia kengele kwenye upindo wa koti. Hivyo, kengele na komamanga vilifuatana kuzunguka upindo wa koti hilo, kama vile Yawe alivyomwamuru Musa. Kisha wakawafumia Haruni na wana wake vizibao vya kitani safi, kitambaa cha kitani safi, kofia za kitani safi, makapitula za kitani safi iliyosokotwa, na mikaba ya kitani safi iliyosokotwa kwa sufu ya rangi ya samawi, ya zambarau na nyekundu na kupambwa vizuri, kama vile Yawe alivyomwamuru Musa. Kisha wakatengeneza pambo la zahabu safi kwa ajili ya taji takatifu na kuchora juu yake kama vile wanavyochora muhuri: Takatifu kwa Yawe. Kisha wakalifunga mbele ya kile kitambaa kwa mukaba wa rangi ya samawi, kama vile Yawe alivyomwamuru Musa. Basi, kazi yote ya hema la mukutano ikamalizika. Waisraeli walifanya yote kama vile Yawe alivyomwamuru Musa. Wakamuletea Musa hema takatifu pamoja na vyombo vyake vyote, vifungio vyake, mbao zake, miti yake, nguzo zake na vikalio vyake; kifuniko cha ngozi za kondoo dume na mbuzi kilichotiwa rangi nyekundu, pazia la Pahali Patakatifu, Sanduku la Agano, miti yake na kiti cha rehema; meza na vyombo vyake vyote, mikate iliyotolewa kwa Mungu; kinara cha taa cha zahabu safi, taa zake, vyombo vyake vyote pamoja na mafuta kwa ajili ya taa hizo; mazabahu ya zahabu; mafuta ya kupakaa, ubani wenye harufu nzuri, na pazia la mulango wa hema; mazabahu ya shaba na wavu wake wa shaba, miti yake na vyombo vyake vyote; bakuli, birika na tako lake; mapazia ya upango, nguzo zake na vikalio vyake; pazia la mulango wa upango, kamba zake na misumari yake; vyombo vyote vilivyohitajika katika kazi ya hema takatifu, ni kusema hema la mukutano; na nguo zote zilizofumwa vizuri kabisa kwa ajili ya kazi ya Pahali Patakatifu, ni kusema nguo takatifu za kuhani Haruni, na za wana wake kwa ajili ya kazi za ukuhani. Waisraeli walifanya kila kitu kama vile Yawe alivyomwamuru Musa. Musa akachunguza kila kitu, akaona kwamba walikuwa wamefanya kila kitu kama vile Yawe alivyoamuru. Hivyo Musa akawabariki. Yawe akamwambia Musa: Katika siku ya kwanza ya mwezi wa kwanza, utasimika hema takatifu la mukutano. Ndani ya hema hilo utaweka lile Sanduku la Agano, kisha weka pazia mbele yake. Utaingiza meza na kupanga vyombo vyake juu. Utaingiza kile kinara vilevile na kuweka taa zake juu yake. Mazabahu ya zahabu ya kufukizia ubani utaiweka mbele ya Sanduku la Agano, kisha utatundika pazia kwenye mulango wa hema takatifu. Ile mazabahu ya kuteketezea sadaka utaiweka mbele ya mulango wa hema takatifu la mukutano. Birika la kunawia utaliweka katikati ya hema la mukutano na mazabahu na kulijaza maji. Utazungusha upango na kutundika pazia kwenye mulango wake. Kisha, utatakasa hema pamoja na vyombo vyake vyote kwa kuvipakaa yale mafuta ya kupakaa, nalo litakuwa takatifu. Halafu, utatakasa mazabahu ya kuteketezea sadaka na vyombo vyake vyote kwa kuipakaa mafuta, nayo itakuwa takatifu kabisa. Birika la kunawia na tako lake vilevile utalitakasa kwa namna hiyohiyo. Utamwita Haruni na wana wake wakuje kwenye mulango wa hema la mukutano, kisha uwanawishe. Utamuvalisha Haruni zile nguo takatifu. Utamupakaa mafuta na kumutakasa, kusudi aweze kunitumikia kama vile kuhani. Utawaita wana wake na kuwavalisha zile kanzu. Kisha uwapakae mafuta kama vile ulivyomupakaa baba yao, kusudi nao vilevile wanitumikie kama makuhani. Kupakwa mafuta huku kutawaingiza katika ukuhani wa kudumu katika vizazi vyao vyote. Basi, Musa alitimiza kwa ukamilifu kabisa maagizo yote ya Yawe. Katika siku ya kwanza ya mwezi wa kwanza mwaka wa pili kisha kutoka Misri, hema takatifu likasimikwa. Musa akaweka vikalio vyake, akainua mbao zake, akashikamanisha miti yake na kusimamisha nguzo zake. Akatandaza pazia juu ya hema takatifu na kuweka kifuniko cha hema juu yake, kama vile alivyoamuriwa na Yawe. Kisha akatwaa vile vibao viwili vya mawe na kuviweka katika lile sanduku. Akapitisha ile miti katika vikomo vya sanduku na kuweka kiti cha rehema juu yake. Kisha akaweka lile Sanduku la Agano ndani ya hema na kutundika pazia, na kwa namna hiyo akafunika Sanduku la Agano, kama vile alivyoamuriwa na Yawe. Akaweka meza ndani ya hema la mukutano, upande wa kaskazini, sehemu ya inje ya pazia, na juu yake akapanga mikate iliyotolewa kwa Yawe, kama vile alivyoamuriwa na Yawe. Akaweka kinara ndani ya hema la mukutano, upande wa kusini, kuelekea meza. Mule, mbele ya Yawe, akawasha taa zake, kama vile alivyoamuriwa na Yawe. Akaweka ile mazabahu ya zahabu katika hema, mbele ya pazia, na kufukiza ubani wenye harufu nzuri juu yake, kama vile alivyoamuriwa na Yawe. Akatundika pazia kwenye mulango wa hema takatifu, akaweka pale kwenye mulango wa hema takatifu mazabahu ya sadaka za kuteketezwa, akatolea juu yake sadaka ya kuteketezwa kwa moto na sadaka ya ngano, kama vile alivyoamuriwa na Yawe. Akaweka birika la kunawia katikati ya hema la mukutano na mazabahu, na kutia maji ya kunawa. Musa, Haruni na wana wake, wote wakanawa mikono na miguu yao mule. Kila mara walipoingia ndani ya hema au walipokaribia ile mazabahu, walinawa, kama vile Musa alivyoamuriwa na Yawe. Kwa mwisho Musa akatengeneza upango kuzunguka hema takatifu na mazabahu na kuweka pazia kwenye mulango wa upango. Hivyo, Musa akakamilisha kazi yote. Kisha, lile wingu likafunika lile hema la mukutano na utukufu wa Yawe ukajaza hema. Musa akashindwa kuingia ndani ya hema la mukutano kwa sababu hilo wingu lilikaa juu yake na utukufu wa Yawe ukajaa mule. Katika safari zao zote Waisraeli hawakuanza safari hata kidogo isipokuwa wakati wingu hilo lilipoinuliwa kutoka juu ya hema. Kama wingu hilo halikuinuliwa wao hawakuanza safari. Walingoja mpaka wakati lilipoinuliwa. Katika safari zao zote, Waisraeli waliweza kuliona lile wingu la Yawe juu ya hema wakati wa muchana na ule moto ukiwaka juu yake usiku. Yawe akamwita Musa na kuongea naye katika hema la mukutano, akamwambia: Uwaambie Waisraeli kwamba kama mutu anapenda kumutolea Yawe sadaka ya nyama, nyama huyo atamuchagua kutoka kundi lake la ngombe, kondoo au mbuzi. Kama sadaka mutu anayotoa ni ya kuteketezwa kwa moto, atamuchagua nyama dume asiyekuwa na kilema kutoka kundi lake, atamutolea mbele ya mulango wa hema la mukutano kusudi apate kukubaliwa na Yawe; ataweka mukono wake juu ya kichwa cha nyama wa sadaka ya kuteketezwa kwa moto, ambayo itakubaliwa kwa ajili ya kumufanyia huyo mutu upatanisho. Kisha, atamuchinja huyo ngombe mbele ya Yawe. Nao makuhani wazao wa Haruni wataichukua damu na kuinyunyizia mazabahu inayokuwa kwenye mulango wa hema la mukutano, pande zake zote. Huyo mutu atachuna huyo nyama wa sadaka ya kuteketezwa na kumukata vipandevipande. Hao makuhani wazao wa Haruni watazipanga kuni juu ya mazabahu na kuwasha moto. Kisha makuhani hao watatwaa vile vipande vya nyama, kichwa na mafuta, na kuviweka juu ya kuni juu ya mazabahu. Lakini matumbotumbo na miguu ya nyama yule vitasafishwa kwa maji. Kuhani atateketeza sadaka yote juu ya mazabahu. Hiyo ni sadaka ya kuteketezwa kwa moto yenye harufu nzuri ya kumupendeza Yawe. Kama sadaka yake ya kuteketezwa ataitwaa katika kundi la kondoo au mbuzi, basi atachagua dume asiyekuwa na kilema. Atamuchinjia upande wa kaskazini wa mazabahu, mbele ya Yawe, hao makuhani wazao wa Haruni watainyunyizia mazabahu damu pande zake zote. Kisha yule mutu atamukata vipandevipande, akivitenga kichwa pamoja na mafuta yake, na kuhani ataviweka kwenye moto juu ya mazabahu. Lakini matumbotumbo na miguu yake atavisafisha kwa maji. Kuhani ataiteketeza yote juu ya mazabahu. Hiyo ni sadaka ya kuteketezwa kwa moto yenye harufu nzuri ya kumupendeza Yawe. Ikiwa anamutolea Yawe sadaka ya kuteketezwa ya ndege, basi, ataleta sadaka yake ya hua au kitoto cha njiwa. Kuhani ataleta ndege huyo kwenye mazabahu, atakongonyoa kichwa chake na kukiteketeza juu ya mazabahu. Damu yake itanyunyiziwa kwenye ubavu wa mazabahu. Kibofu chake pamoja na uchafu wake ataviondoa na kuvitupa upande wa mashariki wa mazabahu ambako majivu yanawekwa. Atamushika mabawa na kumupasua, lakini asimwachanishe vipande viwili. Kisha, kuhani atamuteketeza kwenye mazabahu, juu ya kuni. Hiyo ni sadaka ya kuteketezwa kwa moto yenye harufu nzuri ya kumupendeza Yawe. Mutu yeyote akileta sadaka ya ngano kwa Yawe, sadaka hiyo ikuwe ya unga laini. Atautia mafuta na ubani. Kisha, atawaletea hao makuhani, wazao wa Haruni. Atatwaa mukono mumoja wa unga huo laini wenye mafuta na ubani na kumupelekea kuhani mumoja ambaye atauteketeza juu ya mazabahu ukuwe sadaka ya ukumbusho kwa Yawe. Hiyo ni sadaka ya kuteketezwa kwa moto yenye harufu nzuri ya kumupendeza Yawe. Sehemu inayobaki ya sadaka hiyo ni ya makuhani. Hiyo ni sehemu takatifu kabisa ya sadaka Yawe anayotolewa kwa moto. Kama mutu anamutolea Mungu sadaka ya ngano iliyochomwa kwenye furu, hiyo itakuwa ya mikate isiyotiwa chachu ya unga laini uliochanganywa na mafuta ya zeituni, au ya mikate myembamba isiyokuwa na chachu na isiyopakwa mafuta. Ikiwa sadaka unayotoa ni ya mukate uliokaangwa kwenye kikaango, hiyo itakuwa ya unga laini uliochanganywa na mafuta ya zeituni lakini bila chachu. Mikate hiyo itakatwakatwa na kumiminiwa mafuta. Hiyo ni sadaka ya ngano. Kama sadaka unayotoa ni ya mikate iliyopikwa katika sufuria, hiyo itakuwa ya unga laini na imetiwa mafuta. Utaleta sadaka ya ngano iliyotengenezwa kwa vitu hivyo mbele ya Yawe na kuhani ataipeleka kwenye mazabahu. Kuhani atatwaa sehemu ya sadaka hiyo ikiwa ni sadaka ya ukumbusho na kuiteketeza juu ya mazabahu. Hiyo ni sadaka ya kuteketezwa kwa moto yenye harufu nzuri ya kumupendeza Yawe. Sehemu inayobaki ya sadaka ya ngano, ni ya makuhani. Hiyo ni sehemu takatifu kabisa ya sadaka inayotolewa Yawe kwa moto. Sadaka yoyote ya ngano utakayomuletea Yawe inapaswa kuwa imetengenezwa bila chachu, maana hakuna ruhusa hata kidogo ya kutumia chachu wala asali katika sadaka Yawe anazotolewa kwa moto. Unaweza kumuletea Yawe mazao yako ya kwanza kama sadaka. Lakini hayo hayatatolewa kwenye mazabahu kama harufu ya kumupendeza. Utakoleza sadaka zako zote za ngano kwa chumvi. Usiache hata kidogo kuweka chumvi katika sadaka yako ya ngano, maana chumvi ni kitambulisho cha agano Mungu alilofanya pamoja nanyi. Ukimutolea Yawe sadaka ya mazao yako ya kwanza utaitoa hiyo ikiwa imechomwa katika masuke yake, au utaitoa katika mikate ya kuchomwa iliyotengenezwa kwa ngano iliyosagwa. Utaitia mafuta na kuweka ubani. Hiyo ni sadaka ya ngano. Kuhani atateketeza sehemu ya sadaka hiyo ya ngano iliyopondwa na mafuta pamoja na ubani wake wote, ikuwe sadaka ya ukumbusho. Hiyo ni sadaka Yawe anayotolewa kwa moto. Kama mutu anatoa sadaka ya amani na sadaka yake ni ngombe dume au dike, nyama huyo asikuwe na kilema mbele yangu. Ataweka mukono wake juu ya kichwa cha nyama huyo na kumuchinja kwenye mulango wa hema la mukutano. Hao makuhani wazao wa Haruni watainyunyizia mazabahu damu yake pande zake zote. Mafuta yote yanayofunika na yanayokuwa juu ya matumbotumbo ya nyama wa sadaka hiyo ya amani atayateketeza kama sadaka Yawe anayotolewa kwa moto. Atatoa vilevile zile figo mbili na mafuta yake pamoja na ile sehemu bora ya maini. Wazao wa Haruni wataiteketeza juu ya mazabahu pamoja na sadaka ya kuteketezwa inayokuwa juu ya kuni. Hiyo ni sadaka ya kuteketezwa kwa moto yenye harufu nzuri ya kumupendeza Yawe. Kama sadaka hiyo ya amani unayomutolea Yawe ni kutoka kundi la kondoo au mbuzi, basi achaguliwe dume au dike asiyekuwa na kilema. Kama mutu atatoa mwana-kondoo kuwa sadaka yake, basi atamutolea mbele ya Yawe, akiweka mukono wake juu ya kichwa cha nyama huyo na kumuchinja mbele ya hema la mukutano. Makuhani wazao wa Haruni watanyunyizia mazabahu damu yake pande zake zote. Kisha, kutoka katika sadaka hiyo ya amani Yawe anayotolewa kwa moto, atamutolea sehemu hizi: mafuta yake, mukia muzima wenye mafuta uliokatwa karibu kabisa na uti wa mugongo pamoja na mafuta yote yanayofunika matumbotumbo na mafuta yote yanayokuwa kwenye matumbotumbo, zile figo mbili na mafuta yake pamoja na sehemu bora ya maini. Kuhani ataviteketeza hivyo vyote juu ya mazabahu kama vile chakula Yawe anachotolewa kwa moto. Kama sadaka yake ni mbuzi, basi atamutolea mbele ya Yawe akiweka mukono wake juu ya kichwa cha nyama huyo na kumuchinja mbele ya hema la mukutano. Wazao wa Haruni watanyunyizia mazabahu damu yake pande zake zote. Kisha, atamutolea Yawe mafuta yote yanayofunika matumbotumbo na zile figo mbili na mafuta yake pamoja na sehemu bora ya maini. Kuhani ataviteketeza juu ya mazabahu kama chakula kinachotolewa kwa Yawe kwa moto kutoa harufu ya kumupendeza Mungu. Mafuta yote ni ya Yawe. Ndiyo maana munapaswa kufuata sharti hili siku zote na pahali popote mutakapokaa. Musikule hata kidogo mafuta wala damu. Yawe alimwambia Musa: Uwaambie watu wa Israeli hivi: Kama mutu akitenda zambi bila kukusudia, akifanya kitu kilichokatazwa na amri ya Yawe, atafanya hivi: Ikiwa kuhani ambaye amepakwa mafuta ndiye aliyetenda zambi hata akawatia watu katika kosa, basi huyo atamutolea Yawe ngombe dume muchanga asiyekuwa na kilema akuwe sadaka kwa ajili ya zambi. Ataleta huyo ngombe dume muchanga kwenye mulango wa hema la mukutano, mbele ya Yawe. Ataweka mukono wake juu ya kichwa cha ngombe dume huyo na kumuchinja mbele ya Yawe. Huyo kuhani aliyepakwa mafuta atatwaa sehemu ya damu na kuingia nayo ndani ya hema la mukutano. Atachovya kidole chake katika damu hiyo na kuinyunyiza mara saba mbele ya Yawe upande wa mbele wa pazia la Pahali Patakatifu. Kuhani atatwaa sehemu ya damu na kuipakaa kwenye pembe za mazabahu ya kufukizia ubani wenye harufu nzuri, mbele ya Yawe katika hema la mukutano. Damu inayobaki ataimwanga chini kwenye tako la mazabahu ya kuteketezea sadaka inayokuwa karibu na mulango wa hema la mukutano. Kisha ataondoa mafuta yote ya ngombe huyo: mafuta yanayofunika matumbotumbo, figo mbili na mafuta yanayokuwa juu yake na yale yanayokuwa kwenye kiuno na yale yanayoshikamana na figo na maini. Hizi ni sehemu zilezile zinazoondolewa kwa nyama wa sadaka ya amani. Kuhani ataziteketeza juu ya mazabahu ya kuteketezea sadaka. Lakini ngozi ya huyo ngombe, nyama, kichwa, miguu, matumbotumbo na mavi yake, ni kusema ngombe muzima aliyebakia atamupeleka na kumuteketeza inje ya kambi pahali safi ambapo majivu yanatupwa, naye atamuchoma kwa moto juu ya kuni. Atachomwa kwa moto pale pahali pa kumwangia majivu. Ikiwa Waisraeli wote pamoja wametenda zambi bila kukusudia kwa kufanya kitu kilichokatazwa na amri ya Yawe, mara tu zambi hiyo itakapojulikana, watatoa ngombe dume muchanga akuwe sadaka kwa ajili ya zambi. Watamuleta kwenye hema la mukutano. Wazee wao wataweka mikono yao juu ya kichwa cha huyo ngombe dume, kisha atachinjwa mbele ya Yawe. Yule kuhani aliyechaguliwa kwa kupakwa mafuta ataleta sehemu ya damu ya huyo ngombe dume ndani ya hema la mukutano. Atachovya kidole chake katika hiyo damu na kuinyunyiza mbele ya pazia mara saba, mbele ya Yawe. Kisha, sehemu ya damu atazipakaa kwenye pembe za mazabahu inayokuwa katika hema la mukutano mbele ya Yawe. Damu inayobaki ataimwanga chini kwenye tako la mazabahu ya kuteketezea sadaka inayokuwa karibu na mulango wa hema la mukutano. Mafuta yote ya nyama huyo atayatwaa na kuyateketeza kwenye mazabahu. Kwa hiyo atamufanya ngombe dume huyu kama alivyomufanya yule mwingine wa sadaka kwa ajili ya zambi. Basi, huyo kuhani atawafanyia watu ibada hiyo ya upatanisho kwa ajili ya zambi, nao watasamehewa. Kisha atamutwaa ngombe dume huyu na kumupeleka inje ya kambi na kumuteketeza kwa moto kama vile alivyofanya yule mwingine. Hiyo ni sadaka kwa ajili ya zambi ya jamii. Ikiwa mutawala ametenda zambi bila kukusudia kwa kufanya kitu kilichokatazwa na amri ya Yawe, Mungu wake, na hivyo akakuwa na kosa, mara tu akijulishwa zambi hiyo aliyotenda, ataleta sadaka yake ya beberu asiyekuwa na kilema. Ataweka mukono wake juu ya kichwa cha beberu na kumuchinjia pahali wanapochinjia sadaka za kuteketezwa mbele ya Yawe. Hiyo ni sadaka kwa ajili ya zambi. Kuhani atachovya kidole chake katika damu ya sadaka kwa ajili ya zambi na kuipakaa kwenye pembe za mazabahu ya kuteketezea sadaka. Damu inayobaki ataimwanga chini kwenye tako la mazabahu ya kuteketezea sadaka. Mafuta yote ya beberu huyo atayateketeza juu ya mazabahu, kama vile anavyofanya na mafuta ya nyama wa sadaka ya amani. Kwa hiyo kuhani atamufanyia mutawala ibada hiyo ya upatanisho kwa ajili ya zambi yake, naye atasamehewa. Kama mutu wa kawaida ametenda zambi bila kukusudia, kwa kufanya kitu kilichokatazwa na amri ya Yawe na hivyo akakuwa na kosa, mara tu atakapojulishwa kwamba ametenda zambi, ataleta sadaka ya mbuzi dike asiyekuwa na kilema kwa ajili ya zambi aliyotenda. Ataweka mukono wake juu ya kichwa cha mbuzi huyo wa sadaka ya kuondoa zambi, na kumuchinjia pahali wanapochinjia nyama wa sadaka za kuteketezwa. Kuhani atachovya kidole chake katika damu ya sadaka ya kuondoa zambi na kuipakaa kwenye pembe za mazabahu ya kuteketezea sadaka. Damu iliyobaki ataimwanga chini kwenye tako la mazabahu. Mafuta yote ya mbuzi huyo atayaondoa kama vile anavyoondoa mafuta ya nyama wa sadaka ya amani, naye kuhani atayateketeza juu ya mazabahu, na harufu yake nzuri itamupendeza Yawe. Basi, kuhani atamufanyia yule mutu hiyo ibada ya upatanisho, naye atasamehewa. Ikiwa mutu yule ataleta mwana-kondoo kwa ajili ya sadaka ya zambi, basi, ataleta mwana-kondoo dike asiyekuwa na kilema. Ataweka mukono wake juu ya kichwa cha mwana-kondoo huyo wa sadaka kwa ajili ya zambi na kumuchinjia pahali pale wanapochinjia nyama wa sadaka za kuteketezwa. Kisha kuhani atachovya kidole chake katika damu ya sadaka kwa ajili ya zambi na kuipakaa kwenye pembe za mazabahu ya kuteketezea sadaka. Damu inayobaki ataimwanga chini kwenye tako la mazabahu. Kisha ataondoa mafuta yote kama vile anavyoondoa mafuta ya mwana-kondoo wa sadaka ya amani na kuhani atayateketeza juu ya mazabahu, pamoja na sadaka zinazotolewa kwa Yawe kwa moto. Kuhani atamufanyia ibada ya upatanisho kwa ajili ya zambi yake, naye atasamehewa. Kama mutu yeyote akitakiwa kutoa ushuhuda kwenye baraza juu ya jambo aliloona au kusikia naye akikataa kusema kitu, basi, huo ni uovu na atabeba azabu ya zambi ile. Au kama mutu yeyote kati yenu akijichafua bila kukusudia kwa kugusa kitu chochote kichafu, ikuwe ni muzoga wa nyama wa pori au wa kufugwa au wadudu, atakuwa na kosa. Au mutu akigusa kitu chochote toka kwa mwanadamu kinachohesabiwa kuwa kichafu, kikuwe kile ambacho kinamufanya mutu kuwa muchafu bila kujua, basi, atakapojua atakuwa na kosa. Au, kama mutu akiapa kufanya kitu chochote, chema au kibaya, kama vile watu wanavyofanya bila kufikiri, atakapojua atakuwa na kosa. Basi, mutu akiwa na kosa juu ya mambo hayo lazima akubali zambi yake aliyotenda na kumuletea Yawe sadaka yake kwa ajili ya kosa. Kwa ajili ya zambi aliyotenda ataleta kondoo dike au mbuzi dike kutoka kundi lake amutoe sadaka kwa ajili ya zambi. Naye kuhani atamufanyia ibada ya upatanisho kwa ajili ya zambi yake. Lakini kama hawezi kutoa mwana-kondoo wa sadaka ya kosa kwa ajili ya zambi aliyotenda, basi atamuletea Yawe hua wawili au vitoto viwili vya njiwa, mumoja kwa ajili ya sadaka ya zambi na mwingine kwa ajili ya sadaka ya kuteketezwa kwa moto. Atawaleta kwa kuhani, naye kuhani atamutoa mumoja akuwe sadaka kwa ajili ya zambi kwa kumukongonyoa shingo yake bila kuachanisha kichwa chake. Sehemu ya damu yake ataipakaa pembeni ya mazabahu na ile ingine ataimwanga chini kwenye tako la mazabahu. Hiyo ni sadaka kwa ajili ya zambi. Kisha atamutoa yule wa pili kuwa sadaka ya kuteketezwa kulingana na maagizo. Kuhani atamufanyia yule mutu ibada ya upatanisho kwa ajili ya zambi yake, naye atasamehewa. Ikiwa hawezi kutoa hua wawili au vitoto viwili vya njiwa kama vile sadaka yake kwa ajili ya zambi aliyotenda, basi, ataleta unga kilo moja. Lakini hatautia mafuta wala ubani maana ni sadaka kwa ajili ya zambi. Atamuletea kuhani, naye atatwaa unga huo mukono mumoja na kuuteketeza juu ya mazabahu kama sehemu ya ukumbusho, pamoja na sadaka Yawe anazotolewa kwa moto. Hiyo ni sadaka kwa ajili ya zambi. Basi, kuhani atamufanyia yule mutu ibada ya upatanisho kwa ajili ya zambi, naye atasamehewa. Unga unaobaki utakuwa wa kuhani kama vile inavyofanyika juu ya sadaka ya ngano. Yawe akamwambia Musa: Kama mutu yeyote akikosa kwa kutenda zambi bila kujua juu ya kutokutoa vitu vitakatifu Yawe anavyotolewa, atamuletea kondoo dume asiyekuwa na kilema kutoka kundi lake. Wewe utapima bei yake kulingana na kipimo cha Pahali Patakatifu. Hiyo ni sadaka kwa ajili ya kosa. Zaidi ya hayo, yule mutu atalipa hasara yote aliyosababisha juu ya vitu vitakatifu kwa kuongeza sehemu moja ya tano ya bei yake na kumupatia kuhani yote. Basi, kuhani atamufanyia ibada ya upatanisho kwa ajili ya zambi kwa huyo kondoo dume anayekuwa sadaka kwa ajili ya kosa, naye atasamehewa. Mutu yeyote akitenda zambi bila kujua, kwa kuvunja amri yoyote ya Yawe, yeye ana kosa, na atalipa azabu ya kosa lake. Atamuletea kuhani kondoo dume asiyekuwa na kilema kutoka kundi lake ikiwa na bei sawa na ile ya sadaka ya kosa. Na kuhani atamufanyia ibada ya upatanisho kwa kosa alilofanya, naye atasamehewa. Hiyo ni sadaka ya kosa; yeye ana kosa mbele ya Yawe. Yawe akamwambia Musa: Ikiwa mutu yeyote ametenda zambi na kumwasi Yawe kwa kumudanganya mwenzake juu ya kitu alichomuwekesha au juu ya mapatano au juu ya kumunyanganya au kumwiba mwenzake, au amepata kitu cha mwenzake kilichopotea, akisema kwamba hakukiona, au ameapa uongo juu ya kitu chochote ambacho watu wanafanya na kuwa na kosa, mutu yule akitenda zambi na kuwa na kosa, anapaswa kurudisha kile alichoiba au alichonyanganya, au alichowekeshwa, au kitu cha mwenzake kilichopotea akakipata, au kitu chochote alichoapa kwa uongo. Atalipa kila kitu kikamilifu na kuongeza sehemu moja ya tano ya bei yake. Mara tu atakapojua kosa lake atamurudishia mwenyeji. Kisha atamuletea kuhani kondoo dume au mbuzi dume asiyekuwa na kilema amutolee Yawe sadaka kwa ajili ya kosa. Bei ya nyama huyo itakuwa ile ya kawaida kwa ajili ya kosa. Kuhani atamufanyia ibada ya upatanisho mbele ya Yawe, naye atasamehewa kosa ambalo alikuwa amefanya. Yawe akamwambia Musa: Umupatie Haruni na wana wake maagizo haya: hii ndiyo sheria ya ibada juu ya sadaka ya kuteketezwa kwa moto. Sadaka ya kuteketezwa itakuwa kwenye moto juu ya mazabahu usiku kucha mpaka asubui na moto wake uchochewe, usizimike. Kisha kuhani akiwa amevaa nguo yake ya kitani na kapitula yake ya kitani, atatwaa majivu ya ile sadaka kutoka juu ya mazabahu na kuyaweka kando ya mazabahu. Halafu kisha kubadilisha nguo zake atapeleka yale majivu inje ya kambi pahali panapokuwa safi. Moto wa mazabahu lazima uendelee kuwaka wala usizimike. Kila siku asubui kuhani ataweka kuni kwenye moto huo na juu yake atapanga sadaka ya kuteketezwa, mbele ya kuteketeza mafuta ya sadaka ya amani. Moto utaendelea kuwaka siku zote juu ya mazabahu bila kuzimika hata kidogo. Hii ndio sheria juu ya ibada inayoelekea sadaka ya vyakula. Wazao wa Haruni ndio wanaokuwa na uwezo wa kumutolea Yawe sadaka hiyo juu ya mazabahu. Mumoja wa makuhani atatwaa mukono mumoja wa unga wa sadaka ya vyakula pamoja na mafuta na ubani wote na kuviteketeza juu ya mazabahu kama vile sehemu ya ukumbusho. Harufu yake itamupendeza Yawe. Unga uliobakia Haruni na wazao wake makuhani wataukula bila kutiwa chachu. Wataukula kwenye Pahali Patakatifu katika kiwanja cha hema la mukutano. Usipikwe hata kidogo pamoja na chachu. Nimewapa wao sehemu hiyo kutoka sadaka wanazonitolea kwa moto. Ni sadaka takatifu kabisa kama vile sadaka kwa ajili ya zambi na kwa ajili ya kosa zinavyokuwa. Wazao wanaume wa Haruni ndio peke yao wanaoruhusiwa kula sehemu hiyo maana hiyo imetengwa siku zote kwa ajili yao kutoka sadaka Yawe anazotolewa kwa moto. Yeyote atakayezigusa atakuwa mutakatifu. Yawe akamwambia Musa: Tangu wakati wa kutakaswa kwa Haruni na wazao wake wanapaswa kumutolea Yawe kilo moja ya unga laini kwa siku, nusu moja ya unga huo ataitoa asubui na nusu ingine magaribi. Unga huo utachanganywa na mafuta na kupikwa juu ya kikaango. Kisha utauleta ukiwa vipandevipande na kumutolea Yawe na harufu ya sadaka yake itamupendeza Mungu. Kuhani anayekuwa muzao wa Haruni ambaye amepakwa mafuta kushika nafasi yake atamutolea Yawe sadaka hiyo. Hilo ni agizo la milele. Sadaka yote itateketezwa kwa moto. Sadaka yoyote ya ngano iliyotolewa na kuhani itateketezwa yote; haitakuliwa hata kidogo. Yawe akamwambia Musa: Umwambie Haruni na wana wake kwamba hii ndiyo sheria ya ibada kuelekea sadaka kwa ajili ya zambi, pahali ambapo nyama wa sadaka ya kuteketezwa anapochinjiwa ndipo atakapochinjiwa nyama wa sadaka kwa ajili ya zambi, mbele ya Yawe. Hiyo ni sadaka takatifu kabisa. Kuhani anayetolea sadaka hiyo ndiye atakayeikula. Itakuliwa katika Pahali Patakatifu, kwenye kiwanja cha hema la mukutano. Chochote kitakachogusa nyama hiyo kitakuwa kitakatifu. Nguo yoyote ikidondokewa na damu ya sadaka hiyo, basi, nguo hiyo itafuliwa katika Pahali Patakatifu. Sadaka hiyo ikipikiwa katika vyombo vya udongo, vyombo hivyo vitavunjwa. Lakini ikiwa vyombo hivyo ni vya shaba, basi, vitasafishwa vizuri kwa maji. Wanaoruhusiwa kuikula ni wanaume wa ukoo wa makuhani peke yao kwa vile hiyo ni sadaka takatifu kabisa. Lakini kama damu ya sadaka yoyote kwa ajili ya zambi imeletwa ndani ya hema la mukutano kwa kufanya ibada ya upatanisho katika Pahali Patakatifu, sadaka hiyo itateketezwa kwa moto. Hii ndiyo sheria ya ibada kuelekea sadaka kwa ajili ya kosa. Sadaka hiyo ni takatifu kabisa. Nyama wa sadaka kwa ajili ya kosa atachinjiwa pahali wanapochinjiwa nyama wa sadaka za kuteketezwa kwa moto na damu yake itanyunyizwa juu ya mazabahu pande zake zote. Mafuta yake yote: mafuta ya mukia na yale yanayofunika matumbotumbo yatatolewa na kuteketezwa pamoja na zile figo mbili pamoja na mafuta yake na ile sehemu bora ya maini. Kuhani ataviteketeza juu ya mazabahu kama vile sadaka Yawe anayotolewa kwa moto. Hiyo ni sadaka kwa ajili ya kosa. Wanaoruhusiwa kula sadaka hiyo ni wanaume wa ukoo wa makuhani peke yao; ni sadaka takatifu kabisa. Itakuliwa katika Pahali Patakatifu. Sheria ni moja kuelekea sadaka kwa ajili ya kosa na sadaka kwa ajili ya zambi. Kuhani anayefanya ibada ya upatanisho ndiye atakayeitwaa. Kuhani anayetolea sadaka ya kuteketezwa ya mutu yeyote, atatwaa ngozi ya nyama aliyetolewa. Sadaka yoyote ya ngano iliyopikwa juu ya mafika katika chungu au katika kikaango itakuwa mali ya kuhani anayeitolea. Kila sadaka ya ngano, ikuwe imechanganywa na mafuta au kavu, itakuwa ya wazao wa Haruni na wote wagawanyiwe kwa usawa. Hii ndiyo sheria ya ibada kuelekea sadaka za amani ambazo mutu anaweza kumutolea Yawe. Ikiwa mutu anatoa sadaka hiyo kwa kumushukuru Mungu, basi, ataitoa pamoja na maandazi yasiyotiwa chachu yaliyopakwa mafuta, mikate myembamba iliyopakwa mafuta na maandazi ya unga laini uliochanganywa na mafuta. Pamoja na sadaka yake hiyo ya amani ya kumushukuru Mungu, ataleta maandazi yaliyotiwa chachu. Kutokana na maandazi hayo, atamutolea Yawe andazi moja kutoka kila sadaka. Maandazi hayo yatakuwa ya kuhani anayenyunyizia mazabahu damu ya sadaka za amani. Nyama ya sadaka hiyo ya amani ya kumushukuru Mungu itakuliwa siku hiyohiyo inapotolewa. Hataacha hata sehemu yake mpaka asubui. Lakini kama sadaka hiyo ya amani ni ya kutimiza kiapo au ya mapenzi mema, itakuliwa siku hiyohiyo inapotolewa na sehemu ingine inaweza kukuliwa kesho yake. Lakini nyama yoyote ya sadaka hiyo inayobaki mpaka kwa siku ya tatu itateketezwa. Kama nyama yoyote ya sadaka ya amani inakuliwa kwa siku ya tatu, mutu aliyeitoa hatakubaliwa, wala hiyo sadaka haitapokelewa kwa faida yake. Nyama hiyo ni chukizo na mutu atakayeikula atabeba lazima ya uovu wake. Nyama yoyote inayogusa kitu kinachohesabiwa kuwa kichafu isikuliwe. Nyama hiyo itateketezwa kwa moto. Wote wanaohesabiwa kuwa safi wanaweza kula nyama iliyotolewa sadaka ya amani kwa Yawe. Lakini mutu yeyote anayehesabiwa kuwa muchafu akikula nyama hiyo, atatengwa na watu wake. Mutu yeyote anayegusa kitu chochote kinachohesabiwa kuwa kichafu, au kitu cha mutu kinachohesabiwa kuwa kichafu, au nyama anayehesabiwa kuwa muchafu, au kitu chochote kinahesabiwa kuwa kichafu ambacho ni chukizo, akikula nyama ya sadaka ya amani Yawe aliyotolewa, mutu huyo atatengwa na watu wake. Yawe akamwambia Musa: Uwaambie Waisraeli hivi: Musikule mafuta ya ngombe au ya kondoo au ya mbuzi. Mafuta ya nyama yoyote aliyekufa mwenyewe au ya nyama aliyeuawa na nyama wa pori yanaweza kuwekwa kwa matumizi mengine, lakini musiyakule. Mutu yeyote akikula mafuta ya nyama aliyetolewa kwa Yawe kwa moto, atatengwa na watu wake. Tena, musikule damu yoyote, ikuwe ya ndege au ya nyama pahali popote munapoishi. Mutu yeyote akikula damu yoyote, atatengwa na watu wake. Yawe akamwambia Musa: Uwaambie watu wa Israeli hivi: Mutu yeyote akitoa sadaka ya amani, atamupa Yawe sehemu ya sadaka hiyo. Atamuletea kwa mikono yake mwenyewe kama vile sadaka ya kuteketezwa kwa moto. Ataleta mafuta yake pamoja na kilali ambacho atafanya nacho kitambulisho cha kumutolea Yawe. Kuhani atateketeza mafuta yote juu ya mazabahu, lakini kilali kitakuwa cha Haruni na wana wake makuhani. Muguu wa kuume wa nyuma wa nyama wa sadaka zenu za amani mutamupa kuhani. Muguu huo utakuwa mali ya kuhani anayekuwa muzao wa Haruni anayetolea damu ya sadaka za amani na mafuta yake. Yawe amewaagiza watu wa Israeli watenge kilali hicho na muguu huo wa nyama wa sadaka zao za amani, wamupe kuhani Haruni na wazao wake, maana sehemu hiyo imewekewa kwa hao makuhani milele. Hiyo ndiyo sehemu iliyotengwa kwa ajili ya Haruni na wana wake kutoka katika sadaka Yawe anazotolewa kwa moto, tangu siku walipowekwa kuwa makuhani wa Yawe. Walipotakaswa kwa kupakwa mafuta, Yawe aliamuru Waisraeli wawape sehemu hiyo ya sadaka; hiyo itakuwa siku zote haki yao. Basi, hii ndiyo sheria kuelekea sadaka ya kuteketezwa, sadaka ya vyakula, sadaka kwa ajili ya zambi, sadaka kwa ajili ya kosa, kuelekea kutakaswa na kuelekea sadaka ya amani. Yawe akamupa Musa amri hizi juu ya mulima Sinai siku ile alipowaamuru Waisraeli wamuletee sadaka zao, kule katika jangwa la Sinai. Yawe akamwambia Musa: Utwae Haruni na wana wake na zile nguo takatifu, mafuta ya kupakaa, ngombe wa sadaka kwa ajili ya zambi, kondoo dume wawili, na kitunga cha mikate isiyotiwa chachu. Kisha, ukusanye Waisraeli wote pamoja mbele ya mulango wa hema la mukutano. Musa akafanya kama vile alivyoamuriwa na Yawe. Akakusanya Waisraeli wote pamoja mbele ya mulango wa hema la mukutano. Musa akawaambia: Hili ndilo jambo ambalo Yawe ameamuru lifanyike. Halafu Musa akawaleta Haruni na wana wake na kuwanawisha. Kisha akamuvalisha Haruni koti na kuifunga kwa mukaba, akamuvalisha kanzu, akamuvalisha kizibao na kukifunga kwenye kiuno chake kwa mukaba uliofumwa kwa ufundi. Kisha akaweka kifuko kwenye kifua cha Haruni na ndani ya kifuko hicho akatia mawe ya sheria. Halafu akamuvalisha Haruni kofia na upande wa mbele wa Kofia hiyo akaweka pambo la zahabu, taji takatifu, kama vile Yawe alivyomwamuru. Kisha Musa akatwaa mafuta ya kupakaa, akaipakaa ile hema na vitu vyote vilivyokuwa ndani yake akavitakasa. Akanyunyiza sehemu ya mafuta hayo juu ya mazabahu mara saba, akaipakaa mafuta na vyombo vyake vyote, birika na tako lake kwa kuvitakasa. Vilevile Musa akamupakaa Haruni mafuta juu ya kichwa kwa kumutakasa. Kisha Musa akawaleta wana wa Haruni akawavalisha koti na kuwafunga mikaba kwenye viuno, na kuwavalisha kofia kama vile alivyoamuriwa na Yawe. Kisha Musa akaleta ngombe wa sadaka kwa ajili ya zambi, naye Haruni na wana wake wakaweka mikono yao juu ya kichwa cha ngombe huyo. Musa akamuchinja huyo ngombe, akatwaa damu akapakaa pembe za mazabahu pande zote kwa kidole chake kwa kuitakasa. Kisha akatwaa damu iliyobaki akaimwanga chini kwenye tako la mazabahu ambayo alitakasa kwa kuifanyia ibada ya upatanisho. Kisha, akatwaa mafuta yote yaliyokuwa kwenye matumbotumbo yake, sehemu bora ya maini pamoja na figo zote mbili na mafuta yake na kuviteketeza juu ya mazabahu. Lakini nyama ya ngombe huyo, ngozi yake na mavi yake, akaviteketeza kwa moto inje ya kambi kama vile alivyoamuriwa na Yawe. Kisha, Musa akaleta kondoo dume wa sadaka ya kuteketezwa. Haruni na wana wake wakaweka mikono yao juu ya kichwa cha kondoo huyo. Musa akamuchinja na damu ya kondoo huyo akainyunyizia mazabahu pande zake zote. Akakata huyo kondoo vipandevipande, akaviteketeza pamoja na kichwa chake na mafuta yake. Kisha kusafisha matumbotumbo na miguu kwa maji, Musa akaviteketeza vyote juu ya mazabahu pamoja na sehemu zingine za huyo kondoo kama sadaka ya kuteketezwa. Hiyo ni sadaka inayotolewa kwa moto, yenye harufu ya kumupendeza Yawe. Musa akafanya kama vile alivyoamuriwa na Yawe. Kisha akaleta kondoo dume mwingine, kwa ajili ya utakaso. Haruni na wana wake wakaweka mikono yao juu ya kichwa cha kondoo huyo. Musa akamuchinja. Akatwaa damu ya kondoo huyo na kumupakaa Haruni kwenye incha ya sikio lake la kuume, kidole gumba cha mukono wake wa kuume na cha muguu wake wa kuume. Wana wa Haruni nao wakakuja, naye Musa akawapakaa sehemu ya damu kwenye incha za masikio yao ya kuume, vidole gumba vya mikono yao ya kuume na kwenye vidole gumba vya miguu yao ya kuume. Damu ingine akainyunyizia mazabahu pande zake zote. Kisha, akatwaa mafuta yote, mukia pamoja na mafuta yake, mafuta yote yanayofunika matumbotumbo, sehemu bora ya maini, pamoja na figo zote mbili, mafuta yake na paja la muguu wa kuume wa nyuma wa huyo kondoo dume. Kisha, kwenye kile kitunga cha mikate iliyowekwa mbele ya Yawe akatwaa mukate mumoja usiotiwa chachu, mukate mumoja wenye mafuta na mukate mumoja mudogo, akaviweka vyote juu ya vipande vya mafuta na ule muguu. Musa akaviweka katika mikono ya Haruni na wana wake, nao wakafanya kitambulisho cha kumutolea Yawe. Kisha Musa akatwaa vitu hivyo vyote kutoka mikono yao na kuviteketeza juu mazabahu pamoja na sadaka ya kuteketezwa. Hii ni sadaka ya utakaso, yenye harufu ya kumupendeza Yawe, ni sadaka inayotolewa kwa moto. Kisha Musa akatwaa kile kilali na kufanya kitambulisho cha kumutolea Yawe. Sehemu hiyo ya yule kondoo dume wa utakaso ni mali ya Musa kama vile alivyoamuriwa na Yawe. Halafu Musa akatwaa mafuta ya kupakaa na damu kutoka mazabahu akamunyunyizia Haruni na wana wake hata na nguo zao vilevile. Hivyo Musa akamutakasa Haruni na wana wake pamoja na nguo zao. Musa akamwambia Haruni na wana wake: Mupike ile nyama mbele ya mulango wa hema la mukutano, muikulie pale kwenye mulango pamoja na mukate kutoka katika kitunga chenye sadaka za utakaso. Mufanye kama vile nilivyoamuriwa na Yawe, kwamba sehemu hiyo itakuliwa na Haruni na wana wake. Nyama yoyote au mukate wowote utakaobakia unapaswa kuteketezwa. Hamutatoka inje ya mulango wa hema la mukutano kwa muda wote wa siku saba, ni kusema mpaka muda wenu wa kutakaswa umekwisha, muda ambao utatwaa siku saba. Yawe ameamuru tufanye kama vile tulivyofanya leo kusudi tuwafanyie ibada ya upatanisho. Mutabaki kwenye mulango wa hema la mukutano usiku na muchana kwa muda wa siku saba, mukifanya mambo Yawe aliyoamuru, kama sivyo mutakufa. Ndivyo nilivyoamuriwa na Yawe. Basi, Haruni na wana wake wakafanya mambo yote Yawe aliyoamuru kwa njia ya Musa. Siku ya nane kisha siku saba za kutakaswa, Musa akamwita Haruni na wana wake pamoja na wazee wa Israeli. Musa akamwambia Haruni: Twaa mwana-ngombe dume kwa ajili ya sadaka ya kuondoa zambi na kondoo dume kwa ajili ya sadaka ya kuteketezwa, nyama wote wasikuwe na kilema. Kisha uwatoe sadaka mbele ya Yawe. Uwaambie Waisraeli watwae beberu mumoja kwa ajili ya sadaka ya zambi, na mwana-ngombe mumoja na mwana-kondoo mumoja wote wa umri wa mwaka mumoja na wasiokuwa na kilema kwa ajili ya sadaka ya kuteketezwa, ngombe dume mumoja na kondoo dume mumoja kwa ajili ya sadaka ya amani, wamutolee Yawe sadaka pamoja na sadaka ya unga uliochanganywa na mafuta kwa maana leo Yawe atawatokea. Waisraeli wakaleta vyote hivyo mbele ya hema la mukutano kama vile Musa alivyowaamuru na wote pamoja wakaenda kusimama mbele ya Yawe. Musa akawaambia: Hili ndilo jambo ambalo Yawe aliwaamuru mulifanye kusudi utukufu wake uonekane kwenu. Halafu Musa akamwambia Haruni: Kwenda kwenye mazabahu, utolee pale sadaka yako kwa ajili ya zambi na sadaka ya kuteketezwa na kufanya ibada ya upatanisho kwa ajili yako na kwa ajili ya watu wa Israeli. Kisha tolea pale sadaka za watu na kuwafanyia ibada ya upatanisho kama vile Yawe alivyoamuru. Basi, Haruni akakaribia mazabahu, akachinja yule mwana-ngombe aliyemutoa kuwa sadaka kwa ajili ya zambi yake mwenyewe. Wana wake wakamuletea damu, naye akachovya kidole chake katika damu hiyo na kuipakaa kwenye pembe za mazabahu. Damu iliyobakia akaimwanga kwenye tako la mazabahu. Lakini mafuta na figo akaviteketeza vyote juu ya mazabahu kama vile Yawe alivyomwamuru Musa. Lakini nyama na ngozi akaviteketeza kwa moto inje ya kambi. Kisha Haruni akamuchinja nyama wa sadaka ya kuteketezwa. Wana wake wakamuletea damu, naye akainyunyizia mazabahu pande zote. Kisha wakamuletea sadaka ya kuteketezwa, kipande kimojakimoja, na kichwa, naye akaviteketeza juu ya mazabahu. Akasafisha matumbotumbo na vikanyagio na kuviteketeza pamoja na ile sadaka ya kuteketezwa kwenye mazabahu. Kisha, Haruni akaleta mbele sadaka ya watu. Akatwaa mbuzi wa sadaka ya watu kwa ajili ya zambi, akamuchinja na kumutoa sadaka kwa ajili ya zambi, kama vile alivyofanya kwa yule wa kwanza. Kisha akaleta mbele ile sadaka ya kuteketezwa akatolea sadaka hiyo kulingana na agizo. Kisha akaleta mbele sadaka ya unga akijaza mukono mumoja na kuiteketeza juu ya mazabahu pamoja na sadaka ya kuteketezwa ya kila asubui. Halafu Haruni akamuchinja vilevile ngombe dume na yule kondoo dume wa sadaka za amani kwa ajili ya watu. Wana wake wakamuletea damu ambayo aliinyunyizia mazabahu pande zote. Mafuta ya ngombe dume huyo na kondoo dume, mukia wa kondoo, mafuta yaliyofunika matumbotumbo, figo na sehemu bora ya maini wakayaweka juu ya vilali, naye akaviteketeza kwenye mazabahu. Lakini vile vilali na ule muguu wa nyuma wa kuume, Haruni akafanya navyo kitambulisho cha kumutolea Yawe, kama vile Musa alivyoamuru. Haruni alipomaliza kutolea sadaka zote: sadaka kwa ajili ya zambi, sadaka za kuteketezwa na sadaka za amani, akawainulia watu mikono, akawabariki, kisha akashuka chini. Halafu Musa na Haruni wakaingia ndani ya hema la mukutano; walipotoka wakawabariki watu, nao utukufu wa Yawe ukaonekana kwa watu wote. Yawe akawasha moto ukaiteketeza sadaka ya kuteketezwa na mafuta yaliyokuwa juu ya mazabahu. Watu wote walipoona huo moto wakapiga vigelegele na kuinama uso mpaka chini. Nadabu na Abihu, wana wa Haruni, wakatwaa kila mumoja chetezo chake, wakaweka moto na ubani, wakamutolea Yawe moto usioruhusiwa, ambao haukulingana na agizo la Yawe. Basi, moto ukatokea mbele ya Yawe, ukawateketeza hao vijana, wakakufa mbele yake. Kwa hiyo, Musa akamwambia Haruni: Kwa tukio hili Yawe amekuonyesha maana ya kile alichosema: Nitajionyesha kuwa mutakatifu kati ya wale wanaokuwa karibu nami, nitatukuzwa mbele ya watu wote! Haruni akanyamaza kimya. Basi, Musa akawaita Misaeli na Elisafani, wana wa Uzieli, baba mudogo wa Haruni, akawaambia wakuje kuondoa maiti za wandugu zao kutoka Pahali Patakatifu na kuzipeleka inje ya kambi. Wakatwaa maiti za wandugu zao na kuzipeleka inje ya kambi wakiwa wamevaa nguo zao, kama vile Musa alivyoamuru. Kisha Musa akamwambia Haruni na wana wake, Eleazari na Itamari: Musivuruge nywele zenu wala musipasue nguo zenu kwa kuomboleza, kama sivyo mutakufa na kuwaletea Waisraeli wote pamoja kasirani ya Yawe. Lakini wandugu zenu, ni kusema jamii yote ya Israeli, wanaweza kuomboleza kwa sababu ya moto huo Yawe alioleta. Musitoke inje ya mulango wa hema la mukutano, kama sivyo mutakufa. Maana mafuta ya kupakaa ya Yawe yangali juu yenu. Haruni na wana wake wakafanya kama vile Musa alivyosema. Yawe akaongea na Haruni, akasema: Munapoingia ndani ya hema la mukutano, wewe na wana wako musikunywe divai wala kileo chochote, kama sivyo mutakufa. Hili litakuwa sharti ambalo vizazi vyenu vyote wanapaswa kulifuata siku zote. Munapaswa kuweka tofauti kati ya mambo matakatifu na mambo yasiyokuwa matakatifu, kati ya mambo machafu na yasiyokuwa machafu. Mutawafundisha Waisraeli masharti yote ambayo nimewaambia kwa njia ya Musa. Musa akamwambia Haruni na wana wake waliobakia, Eleazari na Itamari: Mutwae ile sehemu ya sadaka ya vyakula iliyobakia kutoka sadaka Yawe anazotolewa kwa moto. Muikule karibu na mazabahu bila kutiwa chachu kwa sababu ni takatifu kabisa. Mutaikula katika Pahali Patakatifu kwa sababu hiyo ni haki yako na wazao wako kutoka katika sadaka Yawe anazotolewa kwa moto. Hivi ndivyo nilivyoamuriwa. Lakini kilali ambacho wanafanya nacho kitambulisho cha kumutolea Yawe na muguu unaotolewa sadaka kama vile kitambulisho, munaweza kuvikulia pahali popote pasipo kuwa pachafu. Utakula wewe na watoto wako wanaume na wanawake. Vitu hivyo umepewa kama haki yako na ya wazao wako kutoka sadaka za amani za watu wa Israeli. Ule muguu uliotolewa na kilali cha sadaka ya kufanyia kitambulisho cha kumutolea Yawe watavileta pamoja na sadaka za mafuta zinazotolewa kwa moto, kwa kufanya kitambulisho cha kuvitolea mbele ya Yawe, vikuwe sadaka ya kutolewa kwa kitambulisho. Hivyo vitakuwa vyako pamoja na wana wako; ni haki yenu milele kama vile Yawe alivyoamuru. Basi, Musa akachunguza kwa uangalifu juu ya mbuzi mumoja aliyetolewa sadaka kwa ajili ya zambi, akatambua kwamba alikwisha kuteketezwa kwa moto. Hivyo akawakasirikia sana Eleazari na Itamari, wana wa Haruni waliobakia, akawauliza: Kwa nini hamukumukula katika Pahali Patakatifu kwa vile huyo ni kitu kitakatifu kabisa na mulikuwa mumepewa huyo kwa kuondoa kosa ya Waisraeli wote pamoja na kuwafanyia ibada ya upatanisho mbele ya Yawe? Tena, kwa vile damu yake haikuletwa ndani ya Pahali Patakatifu, mulipaswa kumukulia ndani ya Pahali Patakatifu kama vile nilivyoamuru. Haruni akamwambia Musa: Angalia, leo wametolea sadaka yao ya kuondoa zambi na sadaka ya kuteketezwa mbele ya Yawe; hata hivyo mambo haya yamenipata! Tena kama ningekula ile sadaka kwa ajili ya zambi hivi leo, ingekubalika mbele ya Yawe? Musa aliposikia hayo, akafurahi. Yawe akawaambia Musa na Haruni: Wawaambie Waisraeli hivi: Kati ya nyama wote katika dunia, mumeruhusiwa kula nyama yeyote mwenye kwato zinazogawanyika sehemu mbili na ambaye anacheua. Lakini musikule nyama yeyote ambaye anacheua lakini kwato zake hazigawanyiki sehemu mbili, au ambaye kwato zake zimegawanyika lakini hacheui. Musikule ngamia, maana anacheua lakini kwato zake hazigawanyiki sehemu mbili. Kwenu huyo ni muchafu. Musikule wibari. Yeye anacheua lakini kwato zake hazigawanyiki. Kwenu huyo ni muchafu. Musikule sungura. Yeye anacheua lakini kwato zake hazigawanyiki. Kwenu huyo ni muchafu. Musikule nguruwe. Yeye ana kwato zinazogawanyika lakini hacheui. Kwenu huyo ni muchafu. Kwa sababu nyama hao ni wachafu, musikule nyama yao wala musiguse mizoga yao. Samaki yeyote wa bahari au muto mwenye mapezi na magamba, munaweza kumukula. Lakini chochote kinachoishi katika bahari au ndani ya mito, ambacho hakina mapezi wala magamba, maana viumbe vyote vinavyotembea ndani ya maji na viumbe vingine vyote vinavyoishi ndani ya maji ni vichafu kwenu. Viumbe hivyo vitakuwa siku zote vichafu kwenu. Musikule nyama yao, wala musiguse mizoga yao maana ni chafu. Chochote kinachoishi ndani ya maji ambacho hakina mapezi na magamba ni kichafu kwenu. Ndege hawa wote ni wachafu kwenu. Kwa hiyo, musiwakule: tai, furukombe, kipungu, mwewe, aina zote za kozi, aina zote za kibombobombo, mbuni, kirukanjia, dudumizi, aina zote za kipanga, bundi, munandi, bundi kubwa, mumbi, mwari, muderi, korongo, aina zote za koikoi, hudihudi na popo. Wadudu wote wenye mabawa na wanaotembea kwa miguu mine, hao ni wachafu kwenu. Lakini, kati ya wadudu wenye mabawa na wanaotembea kwa miguu mine mirefu kwa kurukia juu ya udongo munaweza kula. Hao ni: kila aina ya nzige, kila aina ya senene, kila aina ya panzi na kila aina ya parare. Lakini wadudu wengine wote wenye mabawa na miguu mine ni wachafu kwenu. Kugusa nyama fulanifulani kunamufanya mutu kuwa muchafu. Yeyote atakayegusa mizoga yao atakuwa muchafu mpaka magaribi. Mutu akitwaa sehemu ya mizoga yake atakuwa muchafu mpaka magaribi na nguo zake zinapaswa kufuliwa. Mutu yeyote akigusa nyama mwenye kwato zinazogawanyika lakini hacheui, mutu yule atakuwa muchafu. Nyama wote wanaotembelea kwa vitanga vyao ingawa wana miguu mine, ni wachafu kwenu na yeyote atakayegusa muzoga wa nyama kama huyo atakuwa muchafu mpaka magaribi. Mutu yeyote anayebeba muzoga atakuwa muchafu mpaka magaribi, naye atasafisha nguo zake. Hao ni wachafu kwenu. Viumbe hivi ni vichafu kwenu: fuko, panya, kila aina ya mujusi, guruguru, kenge, mijusi, mbulu, na kigeugeu. Hao wote ni wachafu kwenu na yeyote atakayegusa mizoga yao, atakuwa muchafu mpaka magaribi. Ikiwa muzoga wa viumbe hao unaangukia kitu chochote, kikuwe ni kifaa cha mbao au nguo au ngozi au gunia au chombo chochote kinachotumiwa kwa kazi yoyote, chombo hicho kitakuwa kichafu mpaka magaribi. Kwa kukifanya kikuwe safi kinapaswa kusafishwa kwa maji. Ikiwa muzoga wake umeangukia chombo cha udongo, basi, kitu chochote kilicho ndani ya chombo hicho ni kichafu na chombo hicho kinapaswa kuvunjwa. Chakula au kinywaji chochote kilichokuwa ndani ya chombo hicho kitakuwa kichafu. Kila kitu ambacho sehemu ya muzoga imekiangukia, kitakuwa kichafu. Ikiwa ni furu au jiko, kinapaswa kuvunjwa. Vitakuwa vichafu navyo ni vichafu kwenu. Hata hivyo, kisima au chemichemi ya maji vitakuwa safi. Lakini kitu chochote kinachogusa muzoga kitakuwa kichafu. Ikiwa sehemu ya muzoga inaangukia mbegu za kupanda, mbegu hizo hazitakuwa chafu. Lakini ikiwa mbegu zimetiwa katika maji kwa kuota na sehemu yoyote ya muzoga ikaziangukia, basi, mbegu hizo ni chafu kwenu. Ikiwa nyama yeyote munayeruhusiwa kula, anakufa mwenyewe, yeyote atakayegusa muzoga wake, atakuwa muchafu mpaka magaribi. Mutu yeyote akikula nyama ya muzoga huo atafua nguo yake na atakuwa muchafu mpaka magaribi. Na yeyote atakayebeba muzoga huo, atafua nguo zake, naye atakuwa muchafu mpaka magaribi. Kiumbe chochote kinachotambaa katika dunia ni chukizo kwenu, musikikule. Chochote kinachotambaa kwa tumbo lake, chochote kinachotembea kwa miguu mine au miguu mingi, musikikule kwa maana ni chukizo. Hivyo musijifanye kuwa chukizo kwa kula viumbe vinavyotambaa na hivyo kujichafua navyo. Kwa sababu mimi ni Yawe, Mungu wenu, mujitakase na kuwa watakatifu kwa maana mimi ni mutakatifu. Wala musijichafue na kitu chochote kinachotambaa juu ya inchi. Kwa sababu ni mimi Yawe niliyewatoa katika inchi ya Misri kusudi nikuwe Mungu wenu; kwa hiyo mukuwe watakatifu kwa maana mimi ni mutakatifu. Hiyo basi, ndiyo sheria kuelekea nyama, ndege na viumbe vyote vyenye uzima ambavyo vinaishi ndani ya maji na inchi kavu, kwa kutia tofauti kati ya kisichokuwa kichafu na kinachokuwa kichafu, kinachoweza kukuliwa na kisichoweza kukuliwa. Yawe akamwambia Musa: Uwaambie watu wa Israeli hivi: Mwanamuke akipata mimba na kuzaa mutoto mwanaume, atakuwa muchafu kwa muda wa siku saba sawa vile anavyokuwa kwa wakati wake wa ugonjwa wa mwezi. Mutoto huyo atatahiriwa katika siku yake ya nane. Kisha mama wa mutoto ataendelea kuwa muchafu kwa muda wa siku makumi tatu na tatu. Wakati huo, asiguse chochote kilichotakaswa wala kuingia Pahali Patakatifu mpaka siku za kutakasika kwake zitakapotimia. Lakini, kama amezaa mutoto mwanamuke, basi, atakuwa muchafu kwa muda wa majuma mawili kama vile inavyokuwa kwa wakati wa ugonjwa wake wa mwezi. Ataendelea katika kutakasika kwake kwa muda wa siku makumi sita na sita. Siku za kutakaswa kwake zitakapotimia, ikuwe amepata mutoto mwanaume au mwanamuke, atamuletea kuhani kwenye mulango wa hema la mukutano mwana-kondoo wa mwaka mumoja kwa ajili ya sadaka ya kuteketezwa na kitoto cha njiwa au hua, kwa ajili ya sadaka ya zambi. Kuhani atamutolea mbele ya Yawe na kumufanyia huyo mama ibada ya upatanisho mbele ya Yawe. Hivyo huyo mwanamuke atakuwa safi kwa ajili ya kutokwa na damu yake. Hii ni sheria inayoelekea mwanamuke yeyote anayezaa mutoto mwanaume au mwanamuke. Kama hawezi kutoa mwana-kondoo, basi, ataleta hua wawili au vitoto viwili vya njiwa; mumoja kwa ajili ya sadaka ya kuteketezwa na mwingine kwa ajili ya sadaka ya zambi. Kuhani atamufanyia mama huyo ibada ya upatanisho, naye atakuwa safi. Yawe akawaambia Musa na Haruni: Ikiwa mutu yeyote atakuwa na kivimba au upele au chunuku juu ya mwili wake, ikionekana kwamba ni ukoma, basi, ataletwa kwa kuhani Haruni au mumoja wa wana wake anayekuwa kuhani. Kuhani atachunguza pahali panapokuwa ugonjwa na ikiwa nywele za pahali pale zimebadilika kuwa nyeupe na ugonjwa wenyewe ukionekana kuwa uko ndani zaidi ya ngozi ya mwili wake, basi, huo ni ukoma. Kuhani akimaliza kumuchunguza, hivyo atatangaza kwamba mutu yule ni muchafu. Lakini ikiwa kipele hicho, ingawa ni cheupe hakikuingia ndani sana ya ngozi na wala nywele za pahali pale hazikubadilika kuwa nyeupe, basi, kuhani atamutenga mutu yule kwa muda wa siku saba. Siku ya saba, kuhani atamwangalia tena mutu yule, na ikiwa, kulingana na uchunguzi wa kuhani, ugonjwa huo haujaenea kwenye ngozi yake, basi, kuhani atamutenga mutu yule kwa siku zingine saba. Kuhani atamuchunguza tena mutu yule siku ya saba. Kama kulingana na uchunguzi wake, ile sehemu ya ugonjwa imefifia na ugonjwa haujaenea, basi, kuhani atamutangaza mutu yule kuwa safi, huo ni upele tu. Mutu huyo atafua nguo zake, naye atakuwa safi. Lakini taka lile likienea kwenye ngozi, nyuma ya mutu yule kujionyesha kwa kuhani kwa ajili ya kutakaswa kwake, basi, atakuja tena kwa kuhani. Kuhani atamwangalia tena, na kama ule upele umeenea kwenye ngozi, basi, kuhani atamutangaza mutu yule kuwa muchafu, huo ni ukoma. Kama mutu ameshikwa na ukoma, ataletwa kwa kuhani. Kuhani atamwangalia na kama kivimba cheupe ambacho kimefanya nywele zake zikuwe nyeupe na kivimba kile kimegeuka kuwa kidonda kibichi, huo ni ukoma wa muda murefu. Kuhani atamutangaza mutu yule kuwa muchafu. Hatamutenga mutu yule kwa uchunguzi maana yeye ni muchafu. Kama ukoma umemushika na umeenea mwili muzima, toka kwenye kichwa mpaka kwenye miguu kama vile kuhani atakavyoona, pale kuhani atamwangalia. Kuhani akiona kwamba ukoma umemwenea mwili muzima, basi, atamutangaza mutu yule kuwa safi kwa sababu mwili umegeuka kuwa mweupe na hivyo mutu yule ni safi. Lakini kukionekana juu ya mwili wa mutu yule kidonda kibichi, basi, mutu yule atakuwa muchafu. Kuhani ataangalia hicho kidonda kibichi na kumutangaza kuwa ni muchafu kwa sababu huo ni ukoma. Lakini hicho kidonda kikigeuka tena kuwa cheupe, mutu yule atarudi kwa kuhani. Kuhani atamwangalia na akiona kwamba kimegeuka kuwa cheupe, basi, atamutangaza mutu yule kuwa safi. Kama mutu ameshikwa na jipu, nalo limepona, lakini pahali pale jipu lilipokuwa pamegeuka kuwa kivimba cheupe au kuwa pekundu lakini peupe, anapaswa kumwonyesha kuhani. Kuhani atamwangalia yule mutu. Kuhani akiona pamekuwa shimo na nywele za pahali pale zimegeuka kuwa nyeupe, basi, kuhani atamutangaza mutu yule kuwa muchafu. Huo ni ugonjwa wa ukoma ambao umetokana na jipu. Lakini kama kuhani akimwangalia yule mutu na kuona kwamba nywele za pahali pale si nyeupe na wala hakuna shimo, lakini pamefifia, basi, atamutenga huyu mutu kwa muda wa siku saba. Kama ugonjwa huo ukienea kwenye ngozi, basi, kuhani atamutangaza mutu yule kuwa muchafu, sehemu hiyo ina ugonjwa. Lakini, kama ile sehemu haijaenea, basi, lile ni kovu la jipu tu. Kuhani atamutangaza mutu yule kuwa safi. Au, ikiwa kuna pahali palipoungua na ile nyama mbichi imegeuka kuwa nyekundu-nyeupe au ni nyeupe, kuhani atapaangalia. Kama akiona kwamba nywele zimegeuka kuwa nyeupe na pana shimo, basi, huo ni ukoma. Ukoma huo umejitokeza kwa njia ya pahali pale palipoungua. Kuhani atamutangaza mutu yule kuwa muchafu, maana ana ugonjwa wa ukoma. Lakini kama kuhani akiona kwamba nywele za pahali pale si nyeupe na hakuna shimo lakini pamefifia, basi, kuhani atamutenga mutu yule kwa muda wa siku saba. Siku ya saba kuhani atamwangalia. Kama umeenea kwenye ngozi, basi, kuhani atamutangaza mutu yule kuwa muchafu, maana ana ugonjwa wa ukoma. Lakini, kama ile alama haijaenea, lakini imefifia, hicho ni kivimba kilichotokana na kuungua. Basi, kuhani atamutangaza mutu yule kuwa safi, maana hilo ni kovu la kuungua. Kama mutu yeyote mwanaume au mwanamuke, ana kidonda juu ya kichwa au kwenye kidevu, kuhani ataangalia ugonjwa huo. Ikiwa kuhani ataona kwamba kuna shimo na nywele ni manjano na nyembamba, basi, atamutangaza mutu yule kuwa muchafu, maana huo ni upele na ni ukoma wa kichwa au wa kidevu. Kama kuhani ataona kwamba hakuna shimo na nywele si nyeusi, basi kuhani atamutenga mutu yule kwa muda wa siku saba. Siku ya saba kuhani ataangalia kile kidonda. Kama kidonda hicho hakijaenea na hakuna nywele zenye rangi ya manjano wala hakuna vipele vyovyote pahali pale, basi, mutu yule atanyoa nywele au ndevu zake. Lakini pahali pale penye vipele hatapanyoa. Kisha kuhani atamutenga mutu yule kwa muda mwingine wa siku saba. Siku ya saba, kuhani ataangalia vile vipele. Ikiwa kuhani ataona kwamba vipele hivyo havikuenea kwenye ngozi na wala havikuingia ndani ya ngozi, basi, atamutangaza mutu yule kuwa safi. Mutu huyo atafua nguo zake, naye atakuwa safi. Lakini ikiwa vipele hivyo vimeenea kisha kutakaswa, mutu yule ataangaliwa na kuhani na ikiwa vimeenea kwenye ngozi, kuhani hatahitaji kutafuta nywele zenye rangi manjano. Mutu yule atakuwa muchafu. Lakini ikiwa kuhani ataona kwamba vile vipele vimepona na nywele nyeusi zimeota pahali pale, basi, vidonda vimepona, basi, mutu yule ni safi. Kuhani atamutangaza mutu yule kuwa safi. Kama mutu yeyote, akuwe mwanaume au mwanamuke, ana alama nyeupe juu ya mwili wake, kuhani atamwangalia mutu yule. Ikiwa kuhani ataona kwamba alama hizo ni nyeupe kidogo, huo ni upele wa kawaida, mutu yule ni safi. Kama mwanaume amepata upaa, yeye ni safi maana ana upaa tu. Ikiwa upaa huo umetanda tangu nyuma mpaka mbele mutu yule ana upaa tu na yuko safi. Lakini kama kwenye kichwa penye upaa au kwenye paji la uso kwenye upaa kuna alama nyekundu-nyeupe, huo ni ukoma unaotokea kwenye upaa wake juu ya kichwa au kwenye paji lake. Kuhani atamwangalia. Ikiwa kuhani ataona kwamba hicho kivimba ni chekundu-cheupe kwenye upaa au kwenye paji lake na unaonekana kama ukoma kwenye ngozi yake, basi, mutu yule ana ukoma, yeye ni muchafu. Kuhani atamutangaza mutu huyo kuwa muchafu. Ugonjwa wake uko kwenye kichwa chake. Mwenye ukoma yeyote atavaa nguo zilizochanika, nywele zake hatazichanuliwa, na mudomo wake wa juu ataufunika na atalalamika akisema: Mimi ni muchafu, mimi ni muchafu. Ataendelea kuwa muchafu kwa muda wote anaokuwa na ugonjwa ule. Yeye ni muchafu, naye atakaa peke yake inje ya kambi. Kama kuna namna ya taka la ukoma kwenye nguo, ikuwe ya sufu au kitani, nguo ile ikuwe imefumwa au imesokotwa kwa kitani au sufu au ni nguo ya ngozi ya aina yoyote, ikiwa taka lile lina rangi ya kijani au nyekundu katika nguo ile, basi, nguo ile ina ukoma. Kwa hiyo ni lazima kumwonyesha kuhani. Kuhani ataangalia taka lile na kuweka nguo ile kando kwa muda wa siku saba. Siku ya saba ataangalia taka lile. Ikiwa taka lile limeenea katika nguo hiyo, ikuwe ni ya kufuma au kusokotwa au ya ngozi au ya ngozi ya aina yoyote, nguo ile ina ukoma. Hivyo nguo ile ni chafu. Kuhani atachoma kwa moto nguo ile maana ina namna ya ukoma wenye kuenea. Kama kuhani ataona kwamba taka halikuenea katika nguo, basi, ataamuru nguo ile ifuliwe na kuwekwa pembeni kwa muda mwingine wa siku saba. Kuhani ataangalia nguo ile kisha kufuliwa. Ikiwa ile alama haijabadilika rangi yake hata ingawa taka halikuenea, basi, nguo ile ni chafu. Nguo ile utaichoma kwa moto, ikuwe alama ile iko nyuma au mbele ya nguo ile. Kama kuhani ataona kwamba ile alama imefifia kisha kufuliwa, basi atakata ile sehemu inayokuwa na namna ya ukoma. Kisha, ikiwa hiyo alama inaonekana tena kisha katika nguo iliyofumwa au iliyosokotwa au katika kitu chochote cha ngozi, basi ukoma umeenea. Kwa hiyo nguo ile utaichoma kwa moto. Lakini nguo ambayo taka limetokea kisha kufuliwa, itafuliwa kwa mara ya pili na hivyo itapata kuwa safi. Hiyo ni sheria juu ya taka la ukoma linalotokea katika nguo ya sufu au kitani au iliyofumwa au iliyosokotwa au ya ngozi. Kwa njia hiyo mutaweza kutia tofauti kati ya nguo isiyokuwa chafu na ile inayokuwa chafu. Yawe akamwambia Musa: Hii ndiyo sheria juu ya mwenye ukoma katika siku ya kutakaswa kwake. Kisha kupona ataletwa kwa kuhani. Kuhani atakwenda kumwangalia yule mutu inje ya kambi. Ikiwa ukoma huo umepona, basi, kuhani ataamuru watu walete ndege wawili safi wanaokuwa wazima, kipande cha muti wa mwerezi, sufu ya rangi nyekundu na tawi la hisopo kwa ajili ya yule mutu atakayetakaswa. Kuhani atawaamuru wachinje ndege mumoja katika chungu chenye maji safi ya chemichemi. Kuhani atatwaa yule ndege mwingine muzima, kipande kile cha mwerezi, sufu ya rangi nyekundu na lile tawi la hisopo na kuvitumbukiza vyote katika damu ya yule ndege aliyechinjwa. Kisha, atamunyunyizia yule mwenye kutakaswa ile damu mara saba, halafu atamutangaza mutu huyo kuwa safi. Atamwacha yule ndege muzima aende zake katika pori inje ya muji. Huyo mutu atafua nguo zake, atanyoa nywele zake, na kuoga, naye atakuwa safi. Nyuma ya hayo atarudi ndani ya kambi, lakini atakaa inje ya hema lake kwa muda wa siku saba. Siku ya saba atanyoa nywele zake zote, ndevu na kope za macho yake. Kisha atafua nguo zake na kuoga, ataoga kwa maji, naye atakuwa safi. Siku ya nane ataleta wana-kondoo dume wawili wasiokuwa na kilema, kondoo dike wa mwaka mumoja asiyekuwa na kilema, kilo tatu za unga laini uliochanganywa na mafuta kwa ajili ya sadaka ya vyakula pamoja na mafuta sehemu moja ya tatu ya litre. Kuhani atakayetakasa mutu huyo atamuleta mbele ya Yawe karibu na mulango wa hema la mukutano pamoja na vitu alivyoleta. Kuhani atatwaa mwana-kondoo dume mumoja na kumutolea sadaka kwa ajili ya kosa pamoja na yale mafuta sehemu moja ya tatu ya litre. Atafanya kitambulisho cha kuvitolea mbele ya Yawe. Kisha atachinja yule mwana-kondoo katika Pahali Patakatifu, wanapochinjia nyama wa sadaka kwa ajili ya zambi na sadaka ya kuteketezwa kwa moto. Sadaka hii kwa ajili ya kosa na vilevile sadaka kwa ajili ya zambi, ni mali ya kuhani. Ni sadaka takatifu kabisa. Kuhani atatwaa sehemu ya damu ya sadaka kwa ajili ya kosa na kumupakaa mutu anayetakaswa katika incha ya sikio lake la kuume na kidole gumba cha mukono wake wa kuume na kidole gumba cha muguu wake wa kuume. Kisha, kuhani atatwaa sehemu ya ile sehemu moja ya tatu ya mafuta na kuyatia katika kigaja cha mukono wake wa kushoto. Atachovya kidole cha mukono wake wa kuume katika mafuta hayo na kumunyunyizia yule mutu anayetakaswa mara saba mbele ya Yawe. Sehemu ya mafuta yanayobaki katika kigaja chake ataipakaa mutu yule anayetakaswa katika incha ya sikio lake la kuume na kidole gumba cha mukono wake wa kuume na kidole gumba cha muguu wake wa kuume, pahali palepale alipomupakaa damu ya sadaka kwa ajili ya kosa. Yale mafuta yaliyobaki atayapakaa yule mutu kwenye kichwa. Hivyo kuhani atamufanyia ibada ya upatanisho mbele ya Yawe. Kuhani atatolea sadaka kwa ajili ya zambi na kumufanyia yule mutu anayetakaswa ibada ya upatanisho kwa kumwondolea uchafu wake. Kisha atachinja mwana-kondoo wa sadaka ya kuteketezwa. Kuhani atatolea ile sadaka ya kuteketezwa na sadaka ya vyakula juu ya mazabahu. Hivyo kuhani atamufanyia yule mutu ibada ya upatanisho, naye atakuwa safi. Lakini ikiwa mutu yule ni masikini, hana uwezo wa kutoa vitu hivyo, basi ataleta mwana-kondoo dume mumoja kuwa malipo ya sadaka kwa ajili ya kosa ambaye atafanyiwa kitambulisho cha kutoa sadaka kwa kumufanyia yule mutu ibada ya upatanisho. Ataleta vilevile kilo moja ya unga laini uliochanganywa na mafuta kwa ajili ya sadaka ya vyakula na mafuta sehemu moja ya tatu ya litre. Ataleta vilevile hua wawili au vitoto viwili vya njiwa kadiri anavyoweza mumoja atakuwa kwa ajili ya sadaka ya zambi na mwingine kwa ajili ya sadaka ya kuteketezwa. Siku ya nane atamuletea kuhani vitu hivyo mbele ya mulango wa hema la mukutano kwa ajili ya utakaso wake mbele ya Yawe. Kuhani atatwaa yule mwana-kondoo dume wa sadaka kwa ajili ya kosa pamoja na yale mafuta sehemu moja ya tatu ya litre na kufanya kitambulisho cha kuvitolea mbele ya Yawe. Atachinja yule mwana-kondoo dume wa sadaka kwa ajili ya kosa. Kuhani atatwaa sehemu ya damu na kumupakaa yule mutu anayetakaswa katika incha ya sikio lake la kuume, katika kidole gumba cha mukono wake wa kuume na kidole gumba cha muguu wake wa kuume. Kuhani atatia sehemu ya mafuta hayo katika kigaja cha mukono wake wa kushoto. Kisha atamunyunyizia yule mutu kwa kidole cha mukono wake wa kuume sehemu ya hayo mafuta yanayokuwa katika kigaja chake cha kushoto mara saba mbele ya Yawe. Kuhani atamupakaa yule mutu anayetakaswa mafuta katika incha ya sikio lake la kuume, kwenye kidole gumba cha mukono wake wa kuume, na kidole gumba cha muguu wake wa kuume. Atamupakaa pahali pale ambapo alimupakaa ile damu ya sadaka kwa ajili ya kosa. Mafuta yanayobakia katika mukono wake atayapakaa yule mutu kwenye kichwa, kwa kumufanyia ibada ya upatanisho mbele ya Yawe. Kisha kuhani atatwaa mumoja wa wale hua au njiwa wawili kadiri mutu yule anavyoweza kuleta. Hua atakuwa kwa ajili ya sadaka ya zambi na mwingine kwa ajili ya sadaka ya kuteketezwa. Pamoja na hao, atatoa sadaka ya vyakula. Kuhani atamufanyia mutu yule ibada ya upatanisho mbele ya Yawe. Hii ndiyo sheria juu ya mutu mwenye ukoma asiyeweza kutoa sadaka za kumutakasa. Yawe akamwambia Musa na Haruni: Mutakapoingia katika inchi ya Kanana ambayo ninawapa kuwa urizi wenu, nami nikifanya namna ya ukoma uote katika ukuta wa nyumba fulani katika inchi mutakayorizi, basi, mwenye nyumba hiyo anapaswa kumwambia kuhani kwamba namna ya taka la ukoma imeonekana katika nyumba yake. Kuhani ataamuru vitu vyote ndani ya nyumba hiyo viondoshwe mbele yeye mwenyewe hajaanza uchunguzi wa taka lile, visipate vyote kutangazwa kuwa vichafu. Kisha kuhani ataingia kwa kuiangalia nyumba hiyo. Atachunguza taka lile. Kama taka lile limeonekana juu ya ukuta na limesababisha madoa ya rangi ya kijani kibichi au nyekundu na kuonekana kuwa yamepenya ndani ya kuta, basi, kuhani atatoka inje kwenye mulango na kufunga nyumba hiyo kwa muda wa siku saba. Siku ya saba kuhani atarudi na kuangalia tena nyumba hiyo. Ikiwa taka lile limeenea katika kuta za nyumba hiyo, kuhani ataamuru mawe yanayokuwa kwenye sehemu zenye taka lile yaondolewe na kutupwa pahali pachafu inje ya muji. Lipu ya ndani ya nyumba hiyo itakwaruzwa na uchafu wake utatupwa pahali pachafu inje ya muji. Kisha watatwaa mawe mapya na kujenga pahali walipobomoa. Nao watapiga nyumba hiyo lipu upya. Ikiwa taka lile litatokea tena kisha kutoa mawe hayo na kukwaruza lipu na kuipiga lipu upya, inapasa kuhani akuje kuichunguza. Ikiwa taka limeenea katika nyumba hiyo, basi huo ni ukoma wenye kuteketeza, nyumba hiyo ni chafu. Nyumba hiyo inapaswa kubomolewa na mawe yake, miti yake na lipu vipelekwe pahali pachafu inje ya muji. Zaidi ya hayo, yeyote atakayeingia ndani ya nyumba hiyo wakati itakapokuwa imefungwa, atakuwa muchafu mpaka magaribi. Yeyote anayelala katika nyumba hiyo au kukulia chakula ndani yake, anapaswa kufua nguo zake. Lakini ikiwa kisha kuchunguza nyumba hiyo, kuhani akiona kwamba taka halikuenea kisha kupigwa lipu, basi, kuhani atatangaza kwamba nyumba hiyo ni safi maana taka limekwisha. Kwa kutakasa nyumba hiyo, mwenye nyumba ataleta ndege wawili pamoja na kipande cha muti wa mwerezi, sufu nyekundu na tawi la hisopo. Atachinja ndege mumoja katika chungu chenye maji safi ya chemichemi. Atatwaa kipande cha mwerezi, tawi la hisopo na ile sufu nyekundu pamoja na yule ndege mwingine anayekuwa muzima na kuvitumbukiza vyote katika damu ya yule ndege aliyechinjwa. Kisha atanyunyizia nyumba hiyo damu mara saba. Hivi ndivyo atakavyotakasa nyumba hiyo kwa damu ya ndege, maji safi ya chemichemi, ndege muzima, kipande cha muti wa mwerezi, tawi la hisopo na ile sufu nyekundu. Yule ndege anayekuwa muzima atamwacha aende zake katika pori inje ya muji. Hivi ndivyo atakavyotakasa nyumba hiyo, nayo itakuwa safi. Hii ndiyo sheria juu ya aina yoyote ya taka la ukoma; taka katika nguo au nyumba, kivimba, jipu au chunuku, kwa kuonyesha ni kitu gani kinachokuwa kichafu na kisichokuwa kichafu. Hiyo ndiyo sheria juu ya taka la ukoma. Yawe akamwambia Musa na Haruni: Uwaambie Waisraeli hivi: Mwanaume yeyote akitokwa na usaha, usaha huo unamufanya kuwa muchafu. Na hii ndiyo sheria juu ya uchafu huo: muda wote anapotokwa na usaha au usaha unapokuwa umezuiwa ndani yake, mutu yule ni muchafu. Kitanda chochote atakacholalia au atakachoikalia, kitakuwa kichafu. Mutu yeyote atakayegusa kitanda cha mutu yule anapaswa kufua nguo zake na kuoga. Atakuwa muchafu mpaka magaribi. Mutu yeyote atakayeikalia kitu chochote mutu huyu mwenye kutokwa na usaha alichoikalia, anapaswa kufua nguo na kuoga. Atakuwa muchafu mpaka magaribi. Mutu yeyote atakayegusa mutu anayetokwa na usaha, anapaswa kufua nguo zake na kuoga; naye atakuwa muchafu mpaka magaribi. Mutu yeyote akitemewa mate na mutu anayetokwa usaha, yule aliyetemewa mate anapaswa kufua nguo zake na kuoga. Atakuwa muchafu mpaka magaribi. Tandiko lolote la nyama ambalo mutu anayetokwa na usaha aliikalia litakuwa chafu. Mutu yeyote atakayegusa kitu chochote mutu huyu alichoikalia atakuwa muchafu mpaka magaribi. Mutu yeyote anayebeba kitu chochote kilichokuwa cha mutu huyu anapaswa kufua nguo zake na kuoga. Atakuwa muchafu mpaka magaribi. Mutu yeyote anayetokwa na usaha akimugusa mutu bila kusafisha kwanza mikono yake na kuoga, aliyeguswa atakuwa muchafu mpaka magaribi. Chombo chochote cha udongo kilichoguswa na mutu anayetokwa na usaha kinapaswa kuvunjwa. Lakini chombo chochote cha mbao kitasafishwa kwa maji. Mwanaume yeyote anayetokwa na usaha akiponywa ugonjwa wake, mutu yule anapaswa kungoja siku saba mbele ya kuondolewa uchafu wake. Atafua nguo zake na kuoga kwa maji ya muto, naye atakuwa safi. Siku ya nane, anapaswa kuleta hua wawili au vitoto viwili vya njiwa mbele ya Yawe kwenye mulango wa hema la mukutano na kumupatia kuhani. Kuhani atatoa hao, mumoja kwa ajili ya sadaka ya zambi na mwingine kwa ajili ya sadaka ya kuteketezwa. Kuhani atamufanyia mutu huyu ibada ya upatanisho mbele ya Yawe na kumwondolea uchafu wake wa kutokwa na usaha. Mwanaume yeyote akitokwa na mbegu za uzazi, anapaswa kuoga mwili muzima kwa maji, naye atakuwa muchafu mpaka magaribi. Nguo yoyote iliyodondokewa mbegu za uzazi au ngozi yoyote iliyoguswa na mbegu zile inapaswa kusafishwa kwa maji na itakuwa chafu mpaka magaribi. Kama mwanaume akilala na mwanamuke na kutokwa na mbegu za uzazi, basi, ni lazima wote wawili waoge kwa maji, nao watakuwa wachafu mpaka magaribi. Mwanamuke yeyote anapokuwa na ugonjwa wa mwezi, atakuwa muchafu kwa muda wa siku saba. Mutu yeyote atakayemugusa mwanamuke yule atakuwa muchafu mpaka magaribi. Kitu chochote anacholalia au kuikalia wakati wa kutengwa kwake kitakuwa kichafu. Mutu yeyote atakayegusa kitanda cha huyo mwanamuke anapaswa kufua nguo zake na kuoga kwa maji. Atakuwa muchafu mpaka magaribi. Mutu yeyote atakayegusa kitu chochote mwanamuke huyo anachoikalia anapaswa kufua nguo zake na kuoga kwa maji, naye atakuwa muchafu mupaka magaribi. Mwanaume yeyote atakayegusa kitu chochote mwanamuke yule alicholalia au kuikalia, atakuwa muchafu mpaka magaribi. Kama mwanaume akilala na mwanamuke huyo na damu ya huyo mwanamuke ikimudondokea huyo mwanaume, basi, mwanaume huyo atakuwa muchafu kwa muda wa siku saba. Kitanda chochote huyu mwanaume atakacholalia kitakuwa kichafu. Kama mwanamuke anatokwa na damu kwa muda wa siku nyingi kuliko vile inavyokuwa kawaida au anatokwa damu wakati usiokuwa wa kawaida yake ya kutokwa damu, basi, ataendelea kuwa muchafu muda wote damu inapomutoka. Kitanda chochote anacholalia wakati ule au kiti chochote anachoikalia, kitakuwa kichafu sawa kama wakati wake wa kutengwa. Mutu yeyote atakayegusa vitu hivyo, atakuwa muchafu na anapaswa kufua nguo zake na kuoga. Atakuwa muchafu mpaka magaribi. Nyuma ya kukauka damu yake mwanamuke huyo atangoja bado siku saba kwa kuwa safi, na nyuma ya muda ule atakuwa safi. Siku ya nane atatwaa hua wawili au vitoto viwili vya njiwa na kumuletea kuhani kwenye mulango wa hema la mukutano. Kuhani atatoa mumoja kwa ajili ya sadaka ya zambi na mwingine kwa ajili ya sadaka ya kuteketezwa. Hivyo kuhani atamufanyia huyo mwanamuke ibada ya upatanisho mbele ya Yawe na kumwondolea uchafu wake wa kutokwa damu. Ndivyo mutakavyotenga Waisraeli na uchafu wao, kusudi wasikufe katika uchafu wao juu ya kuchafua hema langu linalokuwa kati yao. Hiyo ndiyo sheria juu ya mwanaume anayetokwa na usaha na anayetokwa na mbegu za uzazi na kuwa muchafu. Sheria hiyo inaelekea vilevile mwanamuke anayetokwa damu na kuwa muchafu. Sheria hiyo inaelekea mwanaume au mwanamuke yeyote anayetokwa na chochote na vilevile inaelekea mwanaume anayelala na mwanamuke ambaye ni muchafu. Yawe akazungumuza na Musa, kisha kufa kwa wana wawili wa Haruni wakati ule walipomukaribia. Akamwambia: Umwambie ndugu yako Haruni asiingie katika Pahali Patakatifu nyuma ya pazia wakati usiokubaliwa. Asiingie pahali pale maana ndipo nitakapotokea katika wingu juu ya kiti cha rehema. Asipotii, atakufa. Haruni ataingia Pahali Patakatifu akiwa na ngombe dume muchanga kwa ajili ya sadaka ya zambi na kondoo dume kwa ajili ya sadaka ya kuteketezwa kwa moto. Ataoga mwili wote katika maji, kisha atavaa nguo takatifu. Ataingia pahali pale akiwa amevaa nguo takatifu: koti la kitani na atavaa kapitula ya kitani na akiwa amevaa kanzu ya kitani na kujifunga mukaba wa kitani. Atatwaa kutoka watu wa Israeli beberu wawili kwa ajili ya sadaka ya zambi na kondoo dume mumoja kwa ajili ya sadaka ya kuteketezwa. Haruni atatoa huyo ngombe dume kwa sadaka ya kuondoa zambi kwa ajili yake mwenyewe na kufanya ibada ya upatanisho kwa ajili yake mwenyewe na jamaa yake. Kisha, wale beberu wawili atawaweka kwenye mulango wa hema la mukutano. Atawapigia kura hao beberu wawili, kura moja kwa ajili ya Yawe na nyingine kwa ajili ya Azazeli. Ataleta yule beberu ambaye kura ilimwangukia kwa ajili ya Yawe na kumutolea sadaka kwa ajili ya zambi. Lakini yule beberu aliyeangukiwa na kura kwa ajili ya Azazeli atatolewa mbele ya Yawe akiwa muzima. Kwa kufanya ibada ya upatanisho, kuhani atamwacha aende katika jangwa kwa Azazeli, kwa ajili ya zambi za jamii. Haruni atatoa ngombe dume wa sadaka ya zambi kwa ajili yake mwenyewe, na kufanya ibada ya upatanisho kwa ajili yake mwenyewe na kwa ajili ya jamaa yake, kisha atachinja ngombe dume yule wa sadaka ya zambi. Halafu atatwaa chetezo na kutwaa makaa toka kwenye mazabahu mbele ya Yawe na mikono miwili ya ubani uliosagwa vizuri sana na atauleta ndani ya pazia. Kusudi asikufe, ataleta ubani ule mbele ya Yawe na kuutia katika moto kusudi moshi wa ubani ule ufunike kifuniko cha Sanduku la Agano. Atatwaa sehemu ya damu ya yule ngombe dume na kunyunyiza kwa kidole chake upande wa mashariki juu ya kiti cha rehema kisha atainyunyizia mbele ya Sanduku la Agano mara saba kwa kidole chake. Halafu atachinja yule beberu wa sadaka ya zambi kwa ajili ya watu wote. Damu ya mbuzi huyo ataileta ndani ya Pahali Patakatifu Sana na kufanya kama vile alivyofanya na damu ya yule ngombe dume; atainyunyiza juu ya kiti cha rehema, upande wake wa mbele. Hivyo atafanya ibada ya upatanisho kwa ajili ya Pahali Patakatifu kwa sababu ya uchafu, makosa na zambi zote za Waisraeli. Ndivyo atakavyofanya vilevile kwa ajili ya hema la mukutano linalokuwa kati ya watu hao wanaokuwa wachafu. Wakati Haruni anafanya ibada ya upatanisho kwa ajili yake mwenyewe, jamaa yake na jamii nzima ya Israeli, kusikuwe hata mutu yeyote ndani ya hema la mukutano mpaka wakati atakapokuwa amemaliza na kutoka inje. Kisha atatoka na kwenda kwenye mazabahu inayokuwa mbele ya Yawe na kufanya ibada ya upatanisho. Atatwaa sehemu ya damu ya yule ngombe dume na ya yule mbuzi na kupakaa pembe za mazabahu pande zote. Atainyunyizia mazabahu hiyo damu kwa kidole chake mara saba na hivyo ataisafisha na kuitakasa toka uchafu wote wa watu wa Israeli. Kisha Haruni kumaliza kutakasa Pahali Patakatifu, hema la mukutano na mazabahu, ndipo atamutoa yule beberu kwa ajili ya Azazeli, akiwa muzima. Haruni ataweka mikono yake juu ya kichwa cha huyo beberu muzima na kuungama juu yake zambi zote za watu wa Israeli, makosa yao yote na zambi zao zote; naye ataziweka zote juu ya kichwa cha yule mbuzi. Kisha atamwacha huyo beberu aende katika jangwa akipelekwa kule na mutu yeyote anayekuwa tayari. Atamwacha huyo beberu aende katika jangwa, pahali pasipokuwa watu, akiwa amebeba maovu yao yote. Kisha Haruni atarudi ndani ya hema la mukutano, atavua na kuziacha mule zile nguo alizovaa alipoingia katika Pahali Patakatifu Sana. Ataoga mule katika Pahali Patakatifu na kuvaa nguo zake. Atatoka na kutolea sadaka yake ya kuteketezwa, na sadaka ya kuteketezwa ya watu wa Israeli, kwa kufanya ibada ya upatanisho kwa ajili yake mwenyewe na kwa ajili ya watu wote. Mafuta ya sadaka kwa ajili ya zambi atayateketeza juu ya mazabahu. Yule mutu aliyepeleka yule beberu kwa Azazeli kwanza atafua nguo zake na kuoga ndipo atakapoweza kuingia ndani ya kambi. Yule ngombe dume na mbuzi waliotolewa sadaka kwa ajili ya zambi ambao damu yao ilipelekwa katika Pahali Patakatifu kwa kufanya ibada ya upatanisho, watapelekwa inje ya kambi na kuteketezwa kwa moto. Ngozi zao, nyama na mavi yao, vyote vitateketezwa kwa moto. Yule mutu atakayewateketeza atafua nguo zake na kuoga, ndipo atakapoweza kuingia katika kambi. Hili ni sharti la kufuata siku zote: Siku ya kumi ya mwezi wa saba, ninyi wenyewe na hata wageni wanaoishi kati yenu, munapaswa kufunga kula siku hiyo na kuacha kufanya kazi. Mutafanya hivyo kwa sababu siku hiyo ndiyo siku ambayo mutafanyiwa ibada ya upatanisho, musafishwe zambi zenu, nanyi mutakuwa safi mbele ya Yawe. Siku hiyo ni siku ya mapumziko kamili nanyi mutafunga. Hili ni sharti la kufuata siku zote. Kuhani aliyepakwa mafuta na kutakaswa ashike nafasi ya baba yake, ndiye atakayefanya ibada ya upatanisho akiwa amevaa nguo takatifu ya kitani. Atafanya ibada ya upatanisho kwa ajili ya Pahali Patakatifu Sana, kwa ajili ya hema la mukutano, mazabahu, makuhani, na kwa ajili ya jamii nzima ya Israeli. Hili ni sharti la kufuata siku zote. Linapaswa kufuatwa kwa kufanya ibada ya upatanisho kwa ajili ya watu wa Israeli mara moja kila mwaka na kusamehewa zambi zao. Musa akafanya yote kama vile alivyoamuriwa na Yawe. Yawe akamwambia Musa: Uwaambie Haruni, wana wake na watu wote wa Israeli maagizo haya: Kama mutu yeyote kati ya Waisraeli akichinja ngombe au mwana-kondoo au mbuzi ndani au inje ya kambi, bila kumuleta nyama huyo kwenye mulango wa hema la mukutano kwa kumutolea Yawe mbele ya makao yake, mutu yule atakuwa na kosa ya kumwanga damu. Amemwanga damu na atatengwa na watu wake. Agizo hili linalazimisha Waisraeli kuletea Yawe nyama ambao wanawachinja katika mashamba. Wataleta nyama wale kwa kuhani kwenye mulango wa hema la mukutano, naye atawachinja na kumutolea Yawe sadaka za amani. Basi, kuhani atanyunyizia damu kwenye mazabahu ya Yawe inayokuwa kwenye mulango wa hema la mukutano na kuteketeza yale mafuta yakuwe harufu nzuri ya kumupendeza Yawe. Kwa hiyo Waisraeli watakoma kabisa kuwatambikia miungu ya uongo wenye umbo la beberu, jambo ambalo limewafanya wakose uaminifu kwangu. Hili ni sharti la kufuata siku zote katika vizazi vyao vyote. Uwaambie kwamba mutu yeyote kati ya Waisraeli au mugeni anayeishi kati yao, anayetoa sadaka ya kuteketezwa au sadaka ingine, lakini haileti mbele ya mulango wa hema la mukutano kwa kumutolea Yawe, mutu yule atatengwa na watu wake. Kama mutu yeyote wa jamii ya Israeli au mugeni anayeishi kati yao anakula damu yoyote, mimi nitamukasirikia mutu yule aliyekula damu na kumutenga mbali na watu wake. Itakuwa hivyo kwa sababu uzima wa kiumbe uko katika damu. Nimewaagiza kutolea damu kwenye mazabahu kwa kufanya ibada ya upatanisho kwa ajili ya roho zenu, kwa sababu damu inafanya upatanisho, nao uzima uko katika damu. Ndiyo maana nimewaagiza Waisraeli hivi: mutu yeyote kati yenu wala mugeni anayeishi kati yenu asikule damu. Mutu yeyote kati ya Waisraeli au mugeni anayekaa kati yao akienda kuwinda nyama au ndege, anapaswa kumwanga damu chini na kuifunika kwa udongo. Maana, uzima wa kila kiumbe uko katika damu. Ndiyo maana nimewaagiza Waisraeli, wasikule damu ya kiumbe chochote maana uzima wa kiumbe chochote ni damu yake. Yeyote atakayekula damu atatengwa. Mutu yeyote akuwe ni mwenyeji au mugeni, anayekula chochote kilichokufa chenyewe au kilichouawa na nyama wa pori anapaswa kufua nguo zake na kuoga. Atakuwa muchafu mpaka magaribi. Nyuma ya hapo atakuwa safi. Lakini kama hafui nguo zake na kuoga, mutu huyu atabeba lazima ya uovu wake. Yawe akamwambia Musa: Uwaambie watu wa Israeli hivi: Mimi ni Yawe, Mungu wenu. Musifanye kama vile watu wa inchi ya Misri ambako mulikaa wanavyofanya, wala musifanye kama vile watu wa inchi ya Kanana ambako ninawapeleka wanavyofanya. Musifuate desturi zao hata kidogo. Ninyi mutafuata maagizo yangu na kushika masharti yangu. Mimi ni Yawe, Mungu wenu. Munapaswa kushika masharti yangu na maagizo yangu: yule anayeyashika ataishi. Mimi ni Yawe. Mutu yeyote wa Israeli haruhusiwi kumukaribia mwanamuke wa jamaa yake wa karibu kusudi alale naye. Mimi ni Yawe. Usimuvunjie heshima baba yako kwa kulala na mama yako aliyekuzaa. Usimupatishe haya, yeye ni mama yako. Usimuvunjie heshima baba yako kwa kulala na mumoja wa wake zake. Hao ni wamama zako. Usilale na dada yako, akuwe ni dada yako, binti wa baba yako au wa mama yako hata kama alizaliwa katika nyumba au pahali pengine. Usilale na mujukuu wako, mutoto wa mwana wako au binti yako, maana sehemu zao za siri ni kama zako mwenyewe. Usilale na binti aliyezaliwa na muke wa baba yako aliyeolewa na baba yako. Binti huyo ni dada yako. Usilale na shangazi yako, maana huyo ni dada ya baba yako. Usilale na dada ya mama yako, maana huyo ni mama yako mukubwa au mudogo. Usilale na muke wa baba yako mukubwa au mudogo; huyo ni mama yako. Usilale na muke wa mwana wako, huyo ni muke wa mwana wako. Usilale naye. Usilale na muke wa ndugu yako, huyo ni shemeki yako. Ukilala na mwanamuke, basi, usilale naye na binti yake, wala wajukuu zake. Hao ni wandugu. Kuwachanganya ni kufanya uovu. Usimwoe dada ya muke wako wakati muke wako angali anaishi, hiyo itasababisha mapigano. Usilale na mwanamuke anapokuwa na ugonjwa wa mwezi. Usilale na muke wa mwenzako na hivyo kujichafua naye. Usimutoe mutoto wako yeyote kuwa sadaka kwa mungu Moleki maana kufanya hivyo utazarau jina langu mimi Mungu wako. Mimi ni Yawe. Usilale na mwanaume mwenzako kama vile ni mwanamuke. Hilo ni chukizo. Usilale na nyama kusudi usijichafue. Mwanaume au mwanamuke yeyote asifanye hivyo. Kufanya hivyo ni upotovu. Musijichafue kwa kufanya mambo hayo maana kwa sababu ya mambo hayo ninafukuza mataifa yanayokuwa mbele yenu kwa vile wao wanafanya hayo na kujichafua. Inchi yao ilichafuliwa nami nikaiazibu, nayo ikawakataa wakaaji wake. Lakini ninyi na wageni wanaokaa kati yenu munapaswa kushika masharti yangu na maagizo yangu na wala musifanye machukizo hayo. Machukizo hayo yalifanywa na watu waliokaa katika inchi ya Kanana mbele yenu, nao wakachafua inchi. Basi, ninyi musifanye mambo hayo, kama sivyo inchi hiyo itawatapika kama vile ilivyolitapika taifa lililokuwa mbele yenu. Watu wote watakaofanya mambo hayo ya kuchukiza wanapaswa kutengwa mbali na watu wao. Kwa hiyo mushike kwa ukamilifu yote ninayowaagiza. Musifuate tabia zozote ya kuchukiza zilizofanywa na wale walioishi katika inchi mbele yenu, kusudi musijichafue kwa njia yake. Mimi ni Yawe, Mungu wenu. Yawe akamwambia Musa: Uwaambie Waisraeli wote pamoja hivi: Mukuwe watakatifu maana mimi Yawe, Mungu wenu, ni mutakatifu. Kila mumoja wenu anapaswa kuheshimu mama yake na baba yake, na kushika Sabato zangu. Mimi ni Yawe, Mungu wenu. Musigeukie sanamu za miungu, wala musijitengenezee sanamu za kuyeyushwa za miungu. Mimi ni Yawe, Mungu wenu. Munaponitolea mimi Yawe sadaka za amani, mutanitolea kama vile inavyotakiwa kusudi mupate kukubaliwa. Sadaka hiyo inapaswa kuliwa siku hiyohiyo inapotolewa au kesho yake. Chochote kinachobaki mpaka kwa siku ya tatu kinapaswa kuteketezwa kwa moto. Kama sehemu ya nyama yake ikikuliwa siku ya tatu, tendo hilo ni chukizo na sadaka hiyo haitakubaliwa. Naye atakayekula nyama hiyo anapaswa kubeba lazima ya uovu wake kwa sababu amechafua kitu kitakatifu cha Yawe. Mutu huyo atatengwa na watu wake. Utakapovuna mavuno ya inchi yako, usivune kabisa mpaka kwenye mupaka wa shamba wala usirudi nyuma kukusanya mabaki. Musirudie kukusanya kila kitu katika shamba la mizabibu, wala usiokote zabibu zilizoanguka chini. Utawaachia wamasikini na wageni. Mimi ni Yawe, Mungu wenu. Musiibe, musidanganye wala kuambiana uongo. Musiape uongo kwa jina langu na kuchafua jina la Mungu wenu. Mimi ni Yawe. Usimutese mwenzako wala kumwibia. Usikae na mushahara wa mutumishi wako usiku kucha mpaka asubui. Usimulaani kiziwi wala kuweka kizuizi mbele ya kipofu, lakini umwogope Mungu wako. Mimi ni Yawe. Unapotoa hukumu uamue kwa haki, usimupendelee masikini wala kumwogopa mwenye cheo. Lakini hukumu mwenzako kwa haki. Usipitepite hata kidogo ukiwachongea watu wa jamaa yako. Usitie maisha ya mwenzako katika hatari ya kifo kwa maneno yako. Mimi ni Yawe. Usimuchukie ndugu yako ndani ya moyo wako, lakini upatane siku zote na mwenzako kusudi usitende zambi. Usijilipize kisasi au kuwa na kinyongo juu ya wazao wa watu wako lakini umupende mwenzako kama vile unavyojipenda wewe mwenyewe. Mimi ni Yawe. Unapaswa kuyashika masharti yangu. Usiiache mifugo yako ipandiwe na nyama wa aina nyingine. Usipande mbegu za aina mbili katika shamba lako. Usivae nguo iliyofumwa kwa aina mbili za nguo. Mwanaume akilala na mwanamuke mujakazi ambaye amechumbiwa na mwanaume mwingine, lakini bado hajakombolewa wala kupewa uhuru, uchunguzi ufanywe. Lakini wasiuawe kwa sababu mwanamuke huyo hakukuwa bado huru. Mwanaume huyo ataleta mbele ya hema la mukutano sadaka yake ya kondoo dume kwa ajili ya kosa na kunitolea mimi Yawe. Kuhani atamufanyia ibada ya upatanisho kwa kutumia kondoo huyo mbele ya Yawe kwa ajili ya zambi aliyotenda, naye atasamehewa zambi hiyo aliyotenda. Mutakapofika katika inchi ya Kanana na kupanda aina zote za miti ya matunda, matunda hayo hamutayakula. Hamutaruhusiwa kuyakula kwa muda wa miaka mitatu. Katika mwaka wa ine matunda yake yote yatakuwa matakatifu, yatatolewa kuwa sadaka ya sifa, kwa Yawe. Lakini matunda ya kuanzia mwaka wa tano hayo munaweza kuyakula na mavuno yenu yataongezeka. Mimi ni Yawe, Mungu wenu. Musikule nyama yoyote pamoja na damu. Musifanye ulozi wala kuaguza. Musikate kwa kiviringo nywele za pembeni ya kichwa wala kunyoa pembe za ndevu zenu. Musijitie chanjo juu ya mwili wenu kwa ajili ya kuomboleza au kujikatakata chanjo yoyote juu ya mwili. Mimi ni Yawe. Usimuchafue binti yako kwa kumufanya kahaba, inchi nzima isipate kuangukia katika ukahaba na hivyo kujaa uovu. Mutashika Sabato zangu na kuheshimu Pahali pangu Patakatifu. Mimi ni Yawe. Musiwaendee waaguzi wa mizimu wala wachawi kwa kuwaomba wawaaguzie. Mukifanya hivi, mutajichafua. Mimi ni Yawe, Mungu wenu. Unapokuwa mbele ya muzee unapaswa kusimama kwa kumupa heshima yake, nawe umwogope Mungu wako. Mimi ni Yawe. Kama kuna mugeni katika inchi yako usimutendee vibaya. Huyo mugeni anayekaa nawe atakuwa kwako kama vile mwenyeji nawe utamupenda kama vile unavyojipenda mwenyewe, kwa sababu nawe ulikuwa mugeni katika inchi ya Misri. Mimi ni Yawe, Mungu wenu. Usikose kuamua kwa haki juu ya vipimo vya urefu, uzito na ujazo. Munapaswa kutumia mizani ya kweli na vipimo vinavyokuwa vya kweli. Mimi ni Yawe, Mungu wenu, niliyewatoa katika inchi ya Misri. Munapaswa kushika na kutimiza masharti yangu na maagizo yangu. Mimi ni Yawe. Yawe akamwambia Musa: Uwaambie Waisraeli hivi: Mutu yeyote kati ya Waisraeli au mugeni anayekaa kati yenu, akimutoa mutoto wake yeyote kuwa sadaka kwa mungu Moleki, mutu huyu anapaswa kuuawa. Wanainchi wa pale watamwua kwa kumupiga mawe. Mimi mwenyewe nitamukasirikia mutu huyu na kumutenga na watu wake kwa sababu alimutoa mumoja wa watoto wake sadaka kwa mungu Moleki na hivyo akachafua Pahali pangu Patakatifu na jina langu takatifu. Kama wanainchi wa pahali pale hawatamwazibu mutu yule kwa kumwua, mimi mwenyewe nitamukasirikia mutu huyu na jamaa yake. Nitawatenga kutoka watu wao, yeye mwenyewe pamoja na wote waliokosa uaminifu kwangu kwa kumwendea mungu Moleki. Kama mutu yeyote anawaendea waaguzi wa mizimu na wachawi na hivyo kukosa uaminifu kwangu, nitamukasirikia mutu huyu na kumutenga na watu wake. Kwa hiyo, mujitakase mukuwe watakatifu, maana mimi ni Yawe, Mungu wenu. Mushike masharti yangu na kuyatimiza. Mimi ni Yawe ninayewatakasa. Mutu yeyote anayemulaani baba yake au mama yake, anapaswa kuuawa. Amemulaani baba au mama yake, kwa hiyo damu yao itakuwa juu yake mwenyewe. Kama mwanaume akifanya uzinzi na muke wa mwenzake, wote wawili wanapaswa kuuawa. Mwanaume akilala na mumoja wa wake za baba yake, anamupatisha baba yake haya, wote wawili wanapaswa kuuawa. Mwanaume huyo na mwanamuke huyo wote wawili watauawa na damu yao itakuwa juu yao wenyewe. Mwanaume yeyote akilala na muke wa mwana wake, wote wawili wanapaswa kuuawa. Wamefanya machafuko na damu yao itakuwa juu yao wenyewe. Kama mwanaume yeyote akilala na mwanaume mwenzake sawa vile ni mwanamuke, basi, wote wawili wanapaswa kuuawa maana wamefanya jambo linalokuwa chukizo na damu yao itakuwa juu yao wenyewe. Kama mwanaume akioa muke na vilevile kumwoa mama yake, huo ni uovu. Wote watatu wanapaswa kuteketezwa kwa moto maana wamefanya uovu. Mutafanya hivyo kwa kukomesha uovu kati yenu. Kama mwanaume yeyote akilala na nyama anapaswa kuuawa na nyama huyo anapaswa kuuawa. Kama mwanamuke anakaribia nyama na kulala naye, mwanamuke huyo anapaswa kuuawa na nyama huyo vilevile na damu yao itakuwa juu yao wenyewe. Kama mwanaume yeyote akimwoa dada yake, binti ya baba yake au mama yake na binti huyo akakubaliana na mwanaume huyo ambaye ni kaka yake, na kulala naye, hilo ni chukizo. Wanapaswa kutengwa na watu wao maana wamefanya jambo la haya. Huyo mwanaume atabeba lazima ya uovu wake, maana amelala na dada yake. Kama mwanaume akilala na mwanamuke anayekuwa na ugonjwa wa mwezi, wote wawili wanapaswa kutengwa na watu wao; huyo mwanaume amelala na mwanamuke aliyekuwa na ugonjwa wa mwezi, na huyo mwanamuke amefunua mutiririko wa damu yake. Usilale na dada ya mama yako wala na shangazi yako, maana hao ni jamaa yako wa karibu. Wote wanaotenda vile watabeba lazima ya uovu wao. Kama mutu akilala na muke wa baba yake, mukubwa au mudogo, anamupatisha baba yake mukubwa au mudogo haya. Wote wawili watabeba lazima ya zambi yao. Wote wawili watakufa bila watoto. Kama mwanaume akimwoa muke wa ndugu yake, anamupatisha ndugu yake haya, huo ni uchafu; wote wawili watakufa bila watoto. Munapaswa kushika na kutimiza masharti yangu na maagizo yangu yote. Kama sivyo inchi ile ambamo ninawapeleka itawatapika. Musifuate desturi za taifa ninalofukuza mbele yenu. Maana waliyafanya hayo yote, nami nikawachukia sana. Lakini, nimekwisha kuwaambia: Mutarizi inchi yao, mimi ninawapa inchi hiyo ikuwe yenu, inchi inayotiririka maziwa na asali. Mimi ni Yawe, Mungu wenu, niliyewatenga na mataifa mengine. Kwa hiyo, munapaswa kutia tofauti kati ya nyama asiyekuwa muchafu na anayekuwa muchafu, kati ya ndege asiyekuwa muchafu na anayekuwa muchafu. Musijichafue kwa kugusa nyama au ndege au chochote kinachotambaa juu ya udongo ambacho nimekitenga kuwa ni kichafu. Kwa sababu mimi Yawe ni mutakatifu, nami nimewatenga ninyi na mataifa mengine kusudi mukuwe mali yangu, mutakuwa watakatifu. Mwanaume au mwanamuke yeyote anayekuwa mulozi au muchawi, anapaswa kuuawa kwa kupigwa mawe. Damu yao itakuwa juu yao wenyewe. Yawe akamwambia Musa: Uwaambie makuhani, wana wa Haruni, kwamba kusikuwe mutu yeyote kati yao atakayejichafua kwa kugusa maiti ya watu wa jamaa yake, isipokuwa kama ni maiti ya ndugu yake wa karibu, ni kusema mama yake, baba yake, mwana wake, binti yake, ndugu yake au dada yake ambaye (aliyekuwa wa jamaa yake ya karibu), naye hajaolewa bado. Yeye, akiwa mwenye madaraka katika jamaa yake, asijichafue. Wazao wa Haruni wasijinyoe upaa kwa kuomboleza wala wasikate pembe za ndevu zao wala kujichanja chanjo juu ya mwili. Watakuwa watakatifu kwa Mungu wao wala wasichafue jina la Mungu wao. Maana wao ndio wanaotolea zile sadaka Yawe anazopewa kwa moto, ni kusema chakula cha Mungu. Basi, wanapaswa kuwa watakatifu. Kwa sababu kuhani ametakaswa kwa ajili ya Mungu wake, asioe kahaba wala mwanamuke asiyekuwa bikira wala aliyefukuzwa na mume wake. Utamutambua kuhani kuwa aliyetakaswa, maana yeye ndiye anayetolea sadaka ya mukate wa Mungu wako. Utamutambua kuwa mutakatifu, maana mimi Yawe ninayekutakasa wewe ni mutakatifu. Binti wa kuhani yeyote akijichafua kwa kufanya ukahaba, atateketezwa kwa moto maana anamuchafua baba yake. Kuhani Mukubwa ni mukubwa kati ya wandugu zake, naye amemiminiwa mafuta ya kupakaa juu ya kichwa chake, na kutakaswa kusudi avae nguo takatifu. Asiache nywele zake kuwa ovyo wala asipasue nguo zake kwa kuomboleza. Asikaribie maiti wala kujichafua kwa maiti hata kama ni ya baba yake au ya mama yake. Kwa sababu ametakaswa kwa kupakwa mafuta ya Mungu wake juu ya kichwa, basi asiondoke katika Pahali Patakatifu wala asipachafue. Mimi ni Yawe. Kuhani Mukubwa anaweza tu kumwoa binti ambaye ni bikira. Haruhusiwi kuoa mwanamuke mujane, mwanamuke asiyekuwa bikira, wala kahaba. Anapaswa kuoa bikira kutoka watu wake mwenyewe kusudi asichafue watoto wake mwenyewe. Mimi ni Yawe niliyemutakasa. Yawe akamwambia Musa: Umwambie Haruni hivi: Muzao wako yeyote katika vizazi vyote vinavyokuja ambaye ana kilema juu ya mwili, haruhusiwi kukaribia na kunitolea mimi Mungu wake sadaka ya mukate. Mutu yeyote anayekuwa na kilema, kipofu, aliyelemaa, mwenye uso uliokatwakatwa, mwenye kiungo kirefu kuliko kawaida, mwenye muguu au mukono uliovunjika, mwenye kigongo, mutu mufupi kuliko kawaida, asiyeona sawasawa, mwenye kivimba, mwenye upele au mutu anayekuwa towashi, asikaribie kumutolea Mungu mukate wake. Muzao yeyote wa kuhani Haruni mwenye kilema asikaribie kwa kunitolea sadaka za kuteketezwa kwa moto. Kwa vile ana kilema, basi, asikaribie kunitolea mimi Mungu mukate wangu. Mutu huyo anaweza kula mukate wa Mungu wake, vitu vitakatifu na vile vitakatifu kabisa. Lakini asilikaribie lile pazia wala ile mazabahu maana ana kilema, asipate kuchafua Pahali Patakatifu, kwa sababu mimi Yawe ndiye ninayewatakasa. Musa akamwelezea Haruni na wana wake na Waisraeli wote mambo hayo yote. Yawe akamwambia Musa: Umwambie Haruni na wana wake makuhani waheshimu vitu ambavyo Waisraeli wametakasa kwa ajili yangu, kusudi wasichafue jina langu takatifu. Mimi ni Yawe. Uwaambie hivi: Kama mumoja wa wazao wenu katika vizazi vyenu vyote akikaribia vitu vitakatifu ambavyo Waisraeli wamevitakasa kwa ajili yangu mimi Yawe akiwa muchafu, mutu huyu atatengwa nami. Mimi ni Yawe. Mutu yeyote wa kizazi cha Haruni akiwa na ugonjwa wa ukoma au anatokwa usaha asikule vitu vitakatifu mpaka atakapokuwa safi. Mutu yeyote akigusa mutu aliyejichafua kwa kugusa maiti au mutu aliyetokwa na mbegu za uzazi, au akigusa kiumbe chochote chenye kutambaa ambacho kinamufanya mutu kuwa muchafu au mutu ambaye anaweza kumuchafua wa aina yoyote, mutu huyu, atakuwa muchafu mpaka magaribi na haruhusiwi kula vyakula vitakatifu mpaka pale atakapokuwa ameoga. Jua litakapotua ndipo atakapokuwa safi. Nyuma ya pale ataweza kula vyakula vitakatifu maana hicho ndicho chakula chake. Kuhani asikule nyama yoyote ya nyama aliyekufa peke yake au kuuawa na nyama wa pori, kusudi asijichafue. Mimi ni Yawe. Kwa hiyo, makuhani washike agizo langu, kusudi wasifanye zambi na kuuawa. Mimi Yawe ndiye ninayewatakasa. Mutu asiyekuwa wa ukoo wa makuhani haruhusiwi kula chakula kitakatifu. Hata mugeni wa kuhani au mutumishi wake haruhusiwi kula. Lakini kama kuhani amenunua mutumwa kwa kuwa mali yake, basi, yule mutumwa anaruhusiwa kula na vilevile wale waliozaliwa katika nyumba yake. Kama binti ya kuhani ameolewa na mutu asiyekuwa kuhani, haruhusiwi kula sadaka ya vitu vitakatifu. Lakini kama binti ya kuhani ni mujane au amefukuzwa na mume wake na hana mutoto, naye amerudi kwa baba yake na kukaa naye kama vile alipokuwa kijana, basi, anaweza kula chakula cha baba yake. Hata hivyo, mugeni haruhusiwi kula chakula hicho. Kama mutu mwingine akikula chakula kitakatifu bila kujua, basi, atalipa nyongezo ya sehemu moja ya tano pamoja na kipimo sawasawa alichokula na kumurudishia kuhani. Kuhani asichafue vitu ambavyo Waisraeli wamemutolea Yawe na hivyo kufanya watu wabebe sababu ya uovu na makosa yao kwa kula vitu vyao vitakatifu. Mimi Yawe ndiye ninayetakasa vitu hivyo. Yawe akamwambia Musa: Umwambie Haruni na wana wake makuhani na Waisraeli wote hivi: Kama mutu yeyote kati yenu au mugeni yeyote anayeishi katika Israeli akitoa sadaka yake, ikuwe ni ya kutimiza kiapo au sadaka ya mapenzi ya kumutolea Yawe kwa kuteketezwa, kusudi apate kukubalika, atatoa katika ngombe dume au katika kondoo beberu asiyekuwa na kilema. Inakatazwa kutoa chochote kinachokuwa na kilema maana hakitakubaliwa kwa faida yenu. Mutu yeyote anapomutolea Yawe sadaka ya amani kwa kutimiza kiapo au sadaka ya mapenzi kutoka katika kundi lake la mifugo, kusudi akubaliwe anapaswa kuwa nyama mukamilifu, nyama huyo asikuwe na kilema chochote. Usimutolee Yawe nyama yeyote anayekuwa kipofu, kilema, aliyevunjika, anayetokwa na usaha, mwenye upele au ukurutu, wala usiwatoe kuwa sadaka ya kuteketezwa kwa moto juu ya mazabahu ya Yawe. Ngombe dume au mwana-kondoo anayekuwa na kiungo kimoja kirefu au kifupi kuliko kawaida wanaweza kumutoa sadaka ya mapenzi. Lakini huyo usimutoe kuwa sadaka ya kutimiza kiapo. Nyama ambaye kiungo chake cha uzazi kimeumizwa, kimepondwa, kimevunjwa au kimekatwa, usimutolee Yawe wala kumutoa kama vile sadaka katika inchi yako. Wala usipokee kutoka kwa wageni nyama wa namna hiyo na kunitolea mimi Mungu wako kama chakula. Nyama hao wana kilema kwa vile wamekatwa na hawatakubaliwa kwa faida yenu. Yawe akamwambia Musa: Ngombe dume, kondoo dume au beberu akizaliwa atabaki na mama yake kwa siku saba. Lakini tangu siku ya nane anaweza kutolewa kwa Yawe kama sadaka ya kuteketezwa kwa moto. Lakini usichinje ngombe au kondoo siku moja pamoja na kitoto chake. Utakaponitolea mimi Yawe sadaka ya shukrani utaitoa kwa namna ambayo itakufanya ukubaliwe. Nyama huyo ni lazima akuliwe siku hiyohiyo. Musiache kitu mpaka kesho yake asubui. Mimi ni Yawe. Kwa hiyo mutashika na kutimiza amri zangu. Mimi ni Yawe. Musichafue jina langu takatifu, maana ni lazima niheshimiwe kati ya watu wa Israeli. Mimi Yawe ndiye ninayewatakasa. Ni mimi niliyewatoa katika inchi ya Misri kusudi nikuwe Mungu wenu. Mimi ni Yawe. Yawe akamwambia Musa: Uwaambie Waisraeli hivi: Katika sikukuu zangu mimi Yawe ambazo zimepangwa mutakuwa na mukutano mutakatifu. Sikukuu ambazo nimepanga ni hizi: Kutakuwa siku sita za kufanya kazi. Lakini siku ya saba ni Sabato. Siku hiyo ni ya mapumziko, hamutafanya kazi na mutakuwa na mukutano mutakatifu. Siku hiyo ya saba hamutafanya kazi. Hiyo ni Sabato ambayo ni takatifu kwangu mimi Yawe katika makao yenu yote. Sikukuu zingine zangu mimi Yawe ambazo mutakuwa na mukutano mutakatifu zitafanyika katika wakati huu uliopangwa. Magaribi ya siku ya kumi na ine ya mwezi wa kwanza mutafanya kwa heshima yangu mimi Yawe sikukuu ya Pasaka. Siku ya kumi na tano ya mwezi huohuo, sikukuu ya Mikate Isiyotiwa Chachu itaanza. Kwa muda wa siku saba, mutakula mikate isiyotiwa chachu. Katika siku ya kwanza mutakuwa na mukutano mutakatifu. Siku hiyo musifanye kazi. Kwa muda wa siku hizo zote saba mutanitolea mimi Yawe sadaka za kuteketezwa kwa moto. Katika siku ya saba mutafanya mukutano mutakatifu. Musifanye kazi. Yawe akamwambia Musa: Uwaambie Waisraeli hivi: Mutakapoingia katika inchi ambayo ninawapa na kuvuna mazao yake, mutamuletea kuhani muganda wa mavuno ya kwanza. Kuhani atafanya nayo kitambulisho cha kunitolea siku inayofuata siku ya Sabato kusudi mupate kukubaliwa. Siku hiyo munapofanya kitambulisho cha kutoa huo muganda mbele yangu mutanitolea mimi Yawe sadaka ya kuteketezwa ya mwana-kondoo dume wa mwaka mumoja asiyekuwa na kilema. Pamoja na sadaka hiyo, mutatoa sadaka ya vyakula ya kilo mbili za unga laini uliochanganywa na mafuta ambayo mutanitolea mimi Yawe kwa moto, na harufu yake itanipendeza. Sadaka yake ya kinywaji ni litre moja ya divai. Mbele ya siku hiyo ya kuniletea mimi Mungu wenu sadaka hiyo, hamuruhusiwi kula mazao ya kwanza ya mavuno yenu, yakuwe mabichi, yamekaangwa au yemepikwa kuwa mikate. Hili ni sharti la kufuata siku zote katika vizazi vyenu pahali popote mutakapoishi. Mutahesabu majuma saba kamili tangu siku ile inayofuata Sabato ile ambapo mutaleta muganda wa sadaka ya kunitolea kwa kitambulisho mimi Yawe. Katika siku ya makumi tano, siku ya pili ya Sabato ya saba, mutanitolea mimi Yawe sadaka ya vyakula vipya. Kila jamaa italeta mikate miwili ya sadaka ya kutoa kwa kitambulisho mbele yangu mimi Yawe. Kila mukate utatengenezwa kwa kilo mbili za unga laini uliotiwa chachu na huo mutanitolea mimi Yawe ukiwa ni matoleo ya malimbuko yenu. Pamoja na hayo, mutatoa wana-kondoo saba wa mwaka mumoja, mwana-ngombe dume mumoja, na kondoo dume wawili. Nyama hao watakuwa sadaka ya kuteketezwa pamoja na sadaka ya vyakula na sadaka za kinywaji. Harufu ya sadaka hizi itanipendeza mimi Yawe. Mutatoa beberu mumoja wa sadaka kwa ajili ya zambi na wana-kondoo dume wawili wa mwaka mumoja kwa ajili ya sadaka za amani. Kuhani atavipitisha mbele yangu mimi Yawe vikuwe sadaka ya kutoa kwa kitambulisho pamoja na mukate wa mavuno ya kwanza na wale wana-kondoo wawili. Vitu hivyo ni vitakatifu kwa Yawe navyo vitakuwa kwa matumizi ya kuhani tu. Siku hiyohiyo mutatoa tangazo ya mukutano mutakatifu. Musifanye kazi. Hili ni sharti la kufuata milele katika vizazi vyenu vyote, katika makao yenu. Unapovuna mavuno yako katika shamba, usivune kabisa mpaka kwenye mupaka wa shamba lako wala usirudi nyuma kukusanya mabaki. Utawaachia hayo wamasikini na wageni. Mimi ni Yawe, Mungu wenu. Yawe akamwambia Musa: Uwaambie watu wa Israeli hivi: Siku ya kwanza ya mwezi wa saba mutafanya siku ya mapumziko, siku ya ukumbusho itakayotangazwa kwa mulio wa baragumu na kufanya mukutano mutakatifu. Musifanye kazi siku hiyo na munitolee mimi Yawe sadaka ya kuteketezwa kwa moto. Yawe akamwambia Musa: Siku ya kumi ya mwezi huu wa saba ni siku ya upatanisho. Siku hiyo ni siku ya kuwa na mukutano mutakatifu. Mutafunga kula na kutoa sadaka Yawe anazotolewa kwa moto. Musifanye kazi zenu zozote za kawaida siku hiyo. Siku hiyo ni siku ya upatanisho, siku ya kuwafanyia ninyi upatanisho mbele ya Yawe, Mungu wenu. Mutu yeyote asiyefunga kula siku hiyo ni lazima atengwe mbali na watu wake. Mutu yeyote atakayefanya kazi yoyote siku hiyo nitamwangamiza kutoka watu wake. Musifanye kazi: hili ni sharti la kufuata siku zote katika vizazi vyenu, na katika makao yenu yote. Siku hiyo, itakuwa kwenu Sabato ya mapumziko na mutafunga. Siku ya Sabato ni siku ya kumi ya mwezi huo tangu magaribi mpaka magaribi inayofuata. Yawe akamwambia Musa: Uwaambie Waisraeli hivi: Tangu siku ya kumi na tano ya mwezi huo wa saba mutafanya sikukuu ya vibanda kwa muda wa siku saba kwa heshima ya Yawe. Siku ya kwanza ya siku hizo saba, mutakuwa na mukutano mutakatifu na musifanye kazi. Kwa muda wa siku saba mutatoa sadaka Yawe anazopewa kwa moto. Siku ya nane mutakuwa na mukutano mutakatifu na kumutolea Yawe sadaka ya kuteketezwa. Mukutano huo ni mutakatifu. Siku hiyo musifanye kazi. Hizo ndizo sikukuu za Yawe zilizopangwa ambazo mutatoa tangazo kuwe mukutano mutakatifu wa kumutolea Yawe sadaka zinazotolewa kwa moto, sadaka za kuteketezwa na sadaka za vyakula, matoleo na sadaka za kinywaji, kila moja kwa siku yake yenyewe. Sadaka hizo ni pamoja na zile munazonitolea mimi Yawe siku ya Sabato kama vile na sadaka zenu za kawaida, sadaka za kutimiza viapo vyenu, na sadaka zenu za mapenzi munazonitolea mimi Yawe. Kisha kuvuna mashamba yenu mutafanya sikukuu kwa muda wa siku saba, tangu siku ya kumi na tano ya mwezi wa saba. Siku ya kwanza itakuwa siku ya mapumziko na hata siku ya nane. Katika siku ya kwanza mutatwaa matunda ya miti yenu mizuri, matawi ya ngazi, matawi yenye majani mengi na matawi ya miti inayoota kandokando ya muto, nanyi mutafanya sikukuu mbele ya Yawe, Mungu wenu kwa siku saba. Kila mwaka munapaswa kufanya sikukuu hii kwa muda wa siku saba kwa heshima ya Yawe. Hili ni sharti la kufuata siku zote katika vizazi vyenu. Mutaifanya katika mwezi wa saba. Kwa muda wa siku saba mutaishi katika vibanda. Wakaaji wote wa Israeli wataishi katika vibanda wakati huo. Jambo hilo litajulisha vizazi vyenu kwamba nilipowatoa babu zenu katika inchi ya Misri, niliwafanya waishi katika vibanda. Mimi ni Yawe, Mungu wenu. Musa akawatangazia Waisraeli sikukuu za Yawe zilizopangwa. Yawe akamwambia Musa: Uwaamuru watu wa Israeli wakuletee mafuta safi kwa ajili ya taa kusudi taa hiyo iendelee kuwaka siku zote. Haruni ataweka taa hiyo ndani ya hema la mukutano, inje ya pazia la Sanduku la Agano kusudi ipate kuwaka mbele yangu tangu usiku mpaka asubui. Hili ni sharti la kufuata siku zote katika vizazi vyenu. Ataweka hizo taa katika kinara cha taa cha zahabu safi ziwake siku zote mbele ya Yawe. Twaa unga laini, kilo kumi na mbili na kupika mikate kumi na miwili. Mikate hiyo itapangwa kwa mistari miwili juu ya meza ya zahabu safi, kila mustari mikate sita. Kila mustari utautia ubani safi kusudi uambatane na mikate hiyo na kuwa sehemu ya sadaka ya kuteketezwa ya ukumbusho kwa Yawe. Kila siku ya Sabato Haruni ataipanga sawasawa katika mustari mbele yangu mimi Yawe kwa ajili ya watu wa Israeli kama vile agano la milele. Haruni na wazao wake peke yao ndio wanaoruhusiwa kula mikate hiyo maana ni mitakatifu kabisa kwa sababu ni sehemu ya sadaka ninazotolewa mimi Yawe kwa moto. Hiyo ni haki yao milele. Siku moja kukatokea fujo kule katika kambi kati ya Mwisraeli mumoja na kijana mumoja wa mama Mwisraeli lakini baba Mumisri. Yule kijana ambaye mama yake aliitwa Selemoti binti ya Dibri wa kabila la Dani, alitukana Mungu na kuzarau jina lake. Basi watu wakamupeleka kijana kwa Musa, wakamutia katika kifungo mpaka pale watakapofunuliwa mapenzi ya Yawe. Basi, Yawe akamwambia Musa: Umuondoe kijana aliyetukana inje ya kambi, wale wote waliomusikia akitukana waweke mikono yao juu ya kichwa chake, na wote pamoja wamwue kwa kumupiga mawe. Nawe uwaambie Waisraeli kwamba mutu yeyote atakayemulaani Mungu wake atabeba lazima ya zambi yake. Mutu yeyote akuwe ni mwenyeji au mugeni anayemutukana Yawe, wote pamoja watamwua kwa kumupiga mawe. Mutu yeyote anayeua mutu mwingine anapaswa naye kuuawa. Mutu yeyote anayeua nyama wa mwenzake anapaswa kutoa malipo: uzima kwa uzima. Mutu yeyote anayemwumiza mwenzake, anapaswa naye aumizwe sawasawa na vile alivyomwumiza mwenzake, akimuvunja mufupa naye atavunjwa mufupa, jicho kwa jicho, jino kwa jino. Kila mutu anayemwumiza mwenzake anapaswa naye aumizwe kulingana na tendo lake. Anayemwua nyama anapaswa kutoa malipo, lakini mutu yeyote akimwua mutu mwingine anapaswa naye auawe. Sheria hii inaelekea mugeni na mwenyeji. Mimi ni Yawe, Mungu wenu. Basi, Musa akawaambia Waisraeli hayo yote. Wakamupeleka yule mutu aliyelaani Yawe inje ya kambi, wakamwua kwa kumupiga mawe. Ndivyo Waisraeli walivyofanya kama vile Yawe alivyomwamuru Musa. Yawe alimwambia Musa kule juu ya mulima Sinai: Uwaambie Waisraeli hivi: Mutakapofika katika inchi ninayowapa mimi Yawe, kila mwaka wa saba inchi itapumzishwa isilimwe kwa heshima ya Yawe. Kwa muda wa miaka sita mutalima udongo, mutapanda, mutakata matawi ya mizabu yenu na kuvuna mazao yenu. Lakini mwaka wa saba utakuwa ni Sabato ya mapumziko, ni Sabato ya Yawe. Musipande chochote wala kukata matawi ya mizabibu yenu. Chochote kinachoota peke yake musikivune wala kuchuma zabibu kutoka miti isiyokatwa matawi. Huo utakuwa mwaka wa kupumzisha udongo. Hata hivyo mwaka huo wa mapumziko ya inchi utawapatia chakula ninyi wenyewe, watumwa wenu na wajakazi, watumishi na wageni wanaokaa kati yenu. Inchi itakulisha nyama wenu wa kufugwa na nyama wa pori wanaokaa kati yenu. Mutahesabu miaka saba mara saba na jumla yake ni miaka makumi ine na tisa. Kisha, katika siku ya kumi ya mwezi wa saba ambayo ni siku ya kufanyiwa upatanisho mutatuma mutu kupiga baragumu katika inchi yote. Mwaka wa makumi tano mutauheshimu kwa kutangaza uhuru kwa watumwa wote katika inchi. Mwaka huo utakuwa ni sikukuu ya ukumbusho wa miaka makumi tano. Kila mumoja wenu atarudilia mali yake na jamaa yake. Kwa sababu mwaka huo ni wa sikukuu ya ukumbusho wa miaka makumi tano, musipande mbegu au kuvuna chochote kinachoota chenyewe wala kuchuma zabibu kutoka miti musiyokata matawi. Mwaka huo ni wa sikukuu kwenu, utakuwa mwaka mutakatifu. Hivyo mutakula yale yanayoota yenyewe katika mashamba. Katika mwaka huo chochote ambacho kiliuzishwa kinapaswa kirudishwe kwa mwenyeji. Unaponunua au kuuzisha shamba kwa mwenzako usimupunje. Bei ya shamba inapaswa kulingana na miaka mbele ya kurudishwa kwa mwenyeji. Kama miaka ni mingi utaongeza bei na kama miaka hiyo ni michache utapunguza bei, maana bei yake itapimwa kulingana na mazao anayokuuzishia. Musipunjane, lakini, mutamwogopa Mungu wenu. Mimi ni Yawe, Mungu wenu. Kwa hiyo, mutafuata masharti yangu na kutimiza maagizo yangu, kusudi mupate kuendelea kuishi kwa usalama katika inchi. Inchi itatoa mazao yake nanyi mutakula na kushiba na kuishi mule kwa usalama. Lakini labda mutafikiri: Tutakula nini katika mwaka wa saba ijapokuwa haturuhusiwi kupanda wala kuvuna mazao yetu? Basi! Mimi nitabariki inchi katika mwaka wa sita nayo itawapa mazao ya kuwatoshelea kwa miaka mitatu. Mutakapopanda katika mwaka wa nane mutakuwa munakula mazao ya zamani na mutaendelea kula tu hata mwaka wa tisa mutakapoanza tena kuvuna. Musiuzishe mashamba kabisa, maana hiyo ni mali yangu na ninyi ni wageni na wasafiri katika inchi yangu. Ndiyo maana katika inchi yote mutakuwa na utaratibu wa kukomboa mashamba. Kama ndugu yako anakuwa masikini, akiuzisha shamba lake, basi, ndugu yake wa karibu mwenye madaraka ya kulikomboa, atalikomboa. Ikiwa mutu yule hana ndugu mwenye madaraka ya kulikomboa, lakini nyuma akakuwa tajiri na kupata uwezo wa kulikomboa shamba lake, basi, atahesabu miaka tangu alipoliuzisha na kulipa garama zake. Yule mutu aliyelinunua anapaswa kumurudishia. Lakini ikiwa hana uwezo wa kulikomboa, basi, litabaki katika mikono ya yule aliyelinunua mpaka mwaka wa sikukuu ya ukumbusho wa miaka makumi tano. Katika mwaka huo, mali hiyo iachiliwe na kurudishiwa kwa yule mutu aliyeiuzisha. Kama mutu akiuzisha nyumba yake ya kukaa inayokuwa ndani ya muji uliojengewa ukuta, ataweza kuikomboa katika kipindi cha mwaka mumoja tangu alipoiuzisha. Kwa mwaka huo muzima atakuwa na haki ya kuikomboa. Kama nyumba inayokuwa katika muji uliojengewa ukuta haikukombolewa kwa muda wa mwaka mumoja, basi, itakuwa mali ya yule aliyeinunua milele katika vizazi vyao vyote, wala haitarudishwa katika mwaka wa sikukuu ya kukumbuka miaka makumi tano. Lakini nyumba za vijiji ambavyo havikuzungushiwa ukuta zitakuwa chini ya sheria ileile ya mashamba. Nyumba hizo zinaweza kukombolewa katika mwaka mumoja lakini ni lazima zirudishwe kwa wenyeji katika mwaka wa kukumbuka miaka makumi tano. Hata hivyo, nyumba zinazokuwa katika miji Walawi wanayorizi zinaweza kukombolewa wakati wowote. Ikiwa mumoja wa Walawi hatumii haki yake ya kukomboa, basi, nyumba iliyouzishwa ni lazima irudishwe kwa mwenyeji katika mwaka wa kukumbuka miaka makuni tano, maana nyumba zinazokuwa katika miji Walawi wanayorizi wamepewa kama sehemu yao kutoka kwa watu wa Israeli. Lakini mashamba Walawi wanayorizi kwa pamoja, yasiuzishwe, maana huo ni urizi wao wa kudumu. Kama ndugu yako amekuwa masikini hata asiweze kujitunza mwenyewe akiwa pamoja nawe, unapaswa kumutunza aendelee kuishi nawe ndivyo utakavyomutendea mugeni au musafiri anayekuwa kwako. Usimwombe akulipe faida ya namna yoyote. Lakini umwogope Mungu, naye ndugu yako apate kuishi pamoja nawe. Usimukopeshe feza kwa kupata faida au kumupa chakula kusudi akulipe faida. Mimi ni Yawe, Mungu wenu, niliyekutoa kutoka inchi ya Misri kwa kukupa inchi ya Kanana, na kusudi nami nikuwe Mungu wako. Kama ndugu yako anayeishi karibu nawe amekuwa masikini, akijiuzisha kwako, usimufanye akutumikie kama mutumwa. Atakaa nawe kama mutumishi wa kulipwa au kama musafiri. Atakutumikia mpaka kwa mwaka wa kukumbuka miaka makumi tano. Kwa mwaka huo unapaswa kumupa uhuru wake arudi kwa jamaa yake na urizi wa wazee wake, umwache pamoja na jamaa yake. Kwa sababu Waisraeli ni watumishi wangu ambao niliwatoa katika inchi ya Misri, basi, wasiuzishwe kama watumwa. Usimukamate ndugu yako kwa kinguvu, lakini utamwogopa Mungu wako. Juu ya watumwa na wajakazi, unaweza kuwanunua kutoka kwa watu wa mataifa mengine jirani. Unaweza vilevile kununua watumwa kutoka kwa wageni wanaokaa pamoja nawe na jamaa zao waliozaliwa katika inchi yenu, nao watakuwa mali yako. Hao watumwa unaweza kuwapatia watoto wako wakuwe mali yao milele. Hao unaweza kuwafanya watumwa wako, lakini kuelekea ndugu yako Mwisraeli, usimutawale kwa kinguvu. Kama mugeni au musafiri anayekaa kati yenu amekuwa tajiri na ndugu yako akiwa masikini na kujiuzisha kwa huyo mugeni au huyo musafiri au kwa mumoja wa jamaa zao, anaweza kukombolewa kisha kujiuzisha, mumoja wa wandugu zake anaweza kumukomboa. Mujomba wake anaweza vilevile kumukomboa, au binamu yake au ndugu wa karibu katika ukoo wake. Anaweza vilevile kujikomboa yeye mwenyewe kama akiwa tajiri. Yeye akishirikiana na yule aliyemununua, atahesabu miaka tangu alipojiuzisha mpaka mwaka wa kukumbuka miaka makumi tano. Malipo ya kuachiliwa huru kwake italingana na miaka aliyomutumikia. Muda ambao amekuwa mutumwa wa bwana wake utapimwa kama muda wa mutumishi wa kulipiwa. Kama hesabu ya miaka mpaka mwaka wa ukumbusho wa miaka makumi tano ni kubwa zaidi, basi atarudisha sehemu kubwa ya bei aliyolipiwa. Kama miaka michache imepunguka mbele ya kufikia kwa sikukuu ya ukumbusho wa miaka makumi tano, atahesabu sehemu ya bei iliyobaki kulingana na miaka hiyo na kumulipa hayo malipo. Muda wote anapokuwa kwa bwana wake anapaswa kutendewa kama mutumishi wa mushahara kila mwaka. Huyo aliyemununua asimutendee kwa kinguvu. Lakini ikiwa mutu huyu na jamaa yake hakukombolewa kwa njia hizo, basi apewe uhuru wake katika mwaka wa ukumbusho wa miaka makumi tano. Waisraeli ni watumishi wangu, maana niliwatoa katika inchi ya Misri. Mimi ni Yawe, Mungu wenu. Musijitengenezee sanamu za miungu ya uongo, musishike sanamu zao za kuchongwa wala nguzo wala sanamu za mawe yaliyochongwa katika inchi yenu na kuviabudu. Mimi ni Yawe, Mungu wenu. Mushike Sabato zangu na kuheshimu Pahali pangu Patakatifu. Mimi ni Yawe. Kama mukifuata masharti yangu na kushika amri zangu, nitawanyeshea mvua kwa wakati unaofaa, inchi ipate kuzaa mavuno kwa wingi, nayo miti ya mashamba matunda yake. Kupepeta ngano kutaendelea mpaka wakati wa kuvuna zabibu, na mavuno ya zabibu mpaka wakati wa kupanda mbegu. Mutakuwa na chakula tele na kuishi kwa usalama katika inchi yenu. Nitawapa amani katika inchi hata muweze kulala bila kuogopeshwa na chochote. Nitaondoa nyama wakali katika inchi na inchi yenu haitapatwa na vita. Mutafukuza waadui zenu na kuwaua kwa upanga. Watano wenu watafukuza waadui mia moja na mia moja wenu watafukuza waadui elfu kumi. Waadui zenu wataangamia mbele yenu kwa upanga. Nitawarehemu na kuwajalia mupate watoto wengi na kuongezeka. Nami nitaliimarisha agano langu nanyi. Wakati wa mavuno mutakuwa mungali munakula mazao ya zamani. Tena itawapasa kuondoa yaliyobaki kwa kupata nafasi ya kulinda mavuno mapya. Nitaweka makao yangu kati yenu, wala sitawaachilia. Nitatembea kati yenu na kuwa Mungu wenu nanyi mutakuwa watu wangu. Mimi ni Yawe, Mungu wenu, niliyewatoa katika inchi ya Misri kusudi musikuwe watumwa wa Wamisri. Mimi nimevunja nira muliyofungiwa katika shingo lenu na kuwafanya mutembee wima. Lakini kama hamutanisikiliza wala kufuata amri zangu, kama mukizarau masharti yangu na kuchukia kwa roho maagizo yangu mukiacha kutii amri zangu zote na kuvunja agano langu, basi, mimi nitafanya hivi: Nitawapiga kwa kuwaletea hofu kubwa ya rafla, kifua kikubwa na homa itakayowapofusha macho na kuwakondesha. Mutapanda mbegu zenu bila mafanikio maana waadui zenu ndio watakaozikula. Mimi nitawashambulia, nanyi mutapigwa na waadui zenu. Mutatawaliwa na wale wanaowachukia. Mutatishwa na kukimbia hata kama hakuna mutu yeyote anayewafukuza. Na kama hata kisha kuazibiwa hivyo hamutanisikiliza, basi, nitawaazibu mara saba zaidi kwa ajili ya zambi zenu. Kiburi chenu nitakivunja kabisa kwa kufanya mbingu kule juu kuwa ngumu kama chuma na inchi yenu bila mvua ikuwe ngumu kama shaba. Mutatumia nguvu zenu bure maana mashamba yenu hayatatoa mavuno na inchi yenu haitazaa matunda. Kama mukiendelea kunipinga na kukataa kunisikiliza, nitazidisha tena azabu yenu mara saba kadiri ya wingi wa zambi zenu. Nitaleta nyama wakali kati yenu ambao watawanyanganya watoto wenu na kula mifugo yenu na kupunguza hesabu yenu hata njia zenu zigeuke kama jangwa. Kama hata kisha azabu hiyo bado hamunigeukii mimi, lakini munazidi kupingana nami, basi, nami nitapingana nanyi na kuwaazibu mara saba zaidi kwa ajili ya zambi zenu. Nitawaletea upanga ambao utalipiza kisasi juu ya agano mulilovunja. Ninyi mutakimbilia katika miji yenu, lakini nitawaletea ugonjwa mukali na kuwatia katika mikono ya waadui zenu. Chakula chenu nitakipunguza hata wanawake kumi watumie mafika moja tu kwa kupika mikate. Watawagawanyia mukate wenu kwa kipimo. Na hata kisha kula mutaendelea kuwa na njaa tu. Na kama hata kisha hayo yote bado hamutanisikiliza mukiendelea kunipinga, basi nami nitapingana nanyi kwa hasira kali, na kuwaazibu mimi mwenyewe mara saba zaidi kwa ajili ya zambi zenu. Halafu mutakula watoto wenu, wanaume na wanawake. Nitaharibu pahali penu pa ibada kule juu ya milima, nitabomoa mazabahu zenu za kufukizia ubani, na kutupa maiti zenu juu ya sanamu za miungu yenu. Roho yangu itawachukia kabisa. Miji yenu nitaiteketeza, pahali penu patakatifu nitapafanya jangwa na harufu zenu nzuri za sadaka sitazikubali. Nitateketeza inchi yenu hivyo kwamba hata waadui wanaohamia mule watashangaa. Nitawatawanya ninyi kati ya watu wa mataifa na kuchomoa upanga juu yenu. Inchi yenu itakuwa ni ukiwa na miji yenu uharibifu. Ninyi mutakapokuwa katika mikono ya waadui zenu, halafu inchi itafurahia Sabato zake wakati itakapokuwa katika hali ya ukiwa. Inchi itapumzika na kufurahia Sabato zake. Kadiri itakapokuwa katika hali ya ukiwa, itapata sehemu ambayo haikupata katika Sabato zenu mulipokuwa mukiishi mule. Na kwa njia ya wamoja wenu watakaobaki nitaleta woga ndani ya moyo wao, katika inchi ya waadui zao hata jani linalopeperushwa litawakimbiza. Watakimbia kama mutu anayekimbia vita. Watakimbia na kuanguka hata kama hakuna mutu anayewafukuza. Wataangukiana ovyo kama mutu anayekimbia vita hata kama hakuna anayewafukuza. Hamutakuwa na nguvu yoyote kwa kuwashambulia waadui zenu. Mutaangamia kati ya mataifa na inchi za waadui zenu zitawameza. Kama wamoja kati yenu wakibakia katika inchi za waadui zenu watakonda na kuisha kwa sababu ya uovu wao na kwa sababu ya uovu wa wazee wao. Lakini kama wakitubu uovu wao na uovu wa wazee wao juu ya uasi waliotenda juu yangu na vilevile juu ya kupingana kwao nami, wakitambua kwa nini nilipingana nao na kuwapeleka katika inchi ya waadui zao, kama kweli moyo wao mugumu ukinyenyekea na kutubu uovu wao, basi, hapo nami nitakumbuka agano langu na Abrahamu, Isaka na Yakobo na kukumbuka ile inchi niliyowaahidia. Wakati watakapokuwa inje ya inchi yao, inchi hiyo itafurahia Sabato zake hapo itakapokuwa katika hali ya ukiwa. Wakati huo wao watatubu uovu wao wa kuzarau maagizo yangu na kuchukia masharti yangu. Lakini, kwa hayo yote, wanapokuwa katika inchi ya waadui zao, mimi sitawatupa wala kuwachukia hata kuwaangamiza kabisa na kuvunja agano langu. Hapana! Kwa ajili yao nitakumbuka agano nililofanya na wazee wao ambao niliwatoa katika inchi ya Misri, mataifa yakishuhudia, kusudi mimi nikuwe Mungu wao. Mimi ni Yawe. Hayo ndiyo masharti, maagizo na sheria ambazo Yawe aliwapa watu wa Israeli kule kwenye mulima Sinai kwa njia ya Musa. Yawe akamwambia Musa: Uwaambie Waisraeli hivi: Mutu akifanya kiapo cha kumutolea Yawe mwanadamu, mutu huyu anaweza kuondoa kiapo chake kwa kulipa kipimo cha feza kinachokadiriwa kama hivi: Mwanaume wa miaka makumi mbili mpaka miaka makumi sita atakombolewa kwa feza shekeli makumi tano kulingana na kipimo cha Pahali Patakatifu. Kama ni mwanamuke, atakombolewa kwa feza shekeli makumi tatu. Kama mutu huyu ni wa miaka kati ya mitano na makumi mbili atakombolewa kwa feza shekeli makumi mbili kama ni kijana na shekeli kumi za feza kama ni binti. Ikiwa ni mutoto wa umri wa kati ya mwezi mumoja na miaka mitano atakombolewa kwa shekeli tano za feza kama ni kijana na shekeli tatu za feza kama ni binti. Ikiwa mutu huyu umri wake ni zaidi ya miaka makumi sita, bei yake itakuwa ni shekeli kumi na tano za feza, kama ni mwanaume na shekeli kumi za feza kama ni mwanamuke. Lakini ikiwa mutu huyu ni masikini na hawezi kulipa malipo yake, basi, mutu yule atapelekwa kwa kuhani. Kuhani atapima bei yake kulingana na uwezo wa huyo aliyefanya kiapo. Ikiwa kiapo chenyewe kinaelekea nyama wa namna ambayo watu wanamutolea Yawe sadaka, basi nyama huyo anakuwa kitu kitakatifu. Hairuhusiwi kumubadilisha nyama huyo na mwingine yeyote, muzuri kwa mubaya au mubaya kwa muzuri. Kama akimubadilisha na nyama mwingine, wote wawili watakuwa watakatifu. Kama kiapo hicho kinaelekea nyama muchafu wa aina ambayo hairuhusiwi kumutolea Yawe, basi, mutu aliyemutoa, atamuleta kwa kuhani, naye kuhani ataamua bei yake kulingana na uzuri au ubaya wake. Jinsi kuhani atakavyoamua, ndivyo itakavyokuwa. Lakini ikiwa mwenyeji anataka kumukomboa, basi, ataongeza asili mia makumi mbili ya bei ya nyama huyo. Mutu akitakasa nyumba yake kuwa takatifu kwa Yawe, kuhani ataamua bei yake kulingana na uzuri au ubaya wake. Jinsi atakavyoamua, ndivyo itakavyokuwa. Kama huyo mutu aliyeitakasa akitaka kuikomboa hiyo nyumba, basi, ataongeza asili mia makumi mbili ya bei yake, nayo itakuwa mali yake. Mutu akitakasa shamba lake, ambalo ni urizi wake, kwa ajili ya Yawe, basi, bei yake itapimwa kulingana na mbegu zinazotumiwa kwa kupanda shamba hilo. Kwa kila kilo makumi mbili za shayiri bei yake itakuwa shekeli makumi tano za feza. Kama akitakasa shamba lake katika mwaka wa kukumbuka miaka makumi tano, bei yake ilingane na vipimo vyenu. Lakini kama akilitakasa kisha mwaka huo, basi, kuhani ataamua bei yake kulingana na miaka inayobaki kufikia mwaka wa ukumbusho wa miaka makumi tano na bei yake ipunguzwe. Kama mwenyeji akitaka kulikomboa, basi, aongeze asili mia makumi mbili ya bei ya shamba hilo, na kisha litakuwa mali yake. Lakini kama hataki kulikomboa au amemwuzishia mutu mwingine, basi, shamba hilo lisikombolewe tena. Katika mwaka wa ukumbusho wa miaka makumi tano shamba hilo litaachiliwa na kuwa la Yawe milele. Kuhani ndiye atakayelirizi. Kama mutu akitakasa shamba alilonunua, ni kusema sio lake kwa urizi, kuhani ataamua bei ya shamba hilo kwa kulingana na miaka inayobaki kufikia mwaka wa ukumbusho wa miaka makumi tano na mutu huyo atalipa bei yake kama ni kitu kitakatifu kwa Yawe. Lakini katika mwaka wa ukumbusho wa miaka makuni tano, shamba hilo lirudishiwe yule mutu aliyeliuzisha. Kila bei itapimwa kwa kipimo cha uzito cha shekeli kulingana na kipimo cha Pahali Patakatifu: uzito wa gera makumi mbili ni sawa na uzito wa shekeli moja. Hairuhusiwi kumutakasa muzaliwa wa kwanza wa nyama. Kufuatana na sheria, huyo ni wa Yawe, akuwe ni ngombe au kondoo. Kama ni nyama muchafu, mwenyeji atamununua kwa kulingana na jinsi munavyomupima na ataongeza asili mia makumi mbili ya bei ya nyama huyo. Kama hakombolewi, basi atauzishwa kulingana na vipimo vyenu. Lakini kitu chochote kilichotakaswa kwa Yawe, kama ni mutu au nyama au kitu kilichopatikana kwa urizi, hakitauzishwa wala kukombolewa. Chochote kilichotakaswa kwa Yawe ni kitakatifu kabisa. Mutu yeyote aliyetakaswa kwa Yawe asikombolewe. Sharti auawe. Zaka za mazao ikuwe ni ngano au matunda ya miti, yote ni mali ya Yawe. Yote ni takatifu kwa Yawe. Kama mutu akitaka kukomboa zaka yake, atalipa bei yake na kuongeza asili mia makumi mbili ya bei ya zaka hiyo. Kuelekea mifugo, kila nyama wa kumi ni mutakatifu kwa Yawe. Mutu yeyote hana ruhusa ya kuuliza kama nyama huyo ni muzuri au mubaya wala nyama huyo hatabadilishwa na mwingine. Kama akibadilishwa na mwingine, nyama wote wawili watakuwa watakatifu. Hawatakombolewa. Hizo ndizo amri ambazo Yawe alimwamuru Musa kusudi awaambie Waisraeli kwenye mulima Sinai. Katika siku ya kwanza ya mwezi wa pili, mwaka wa pili nyuma ya watu wa Israeli kutoka Misri, Yawe akasema na Musa ndani ya hema la mukutano katika jangwa la Sinai, akamwambia hivi: Wewe na Haruni mufanye hesabu ya Waisraeli wote na kuandika majina ya wanaume wote, kulingana na ukoo na jamaa zao. Wale wote katika Israeli wanaoweza kwenda kwa vita, wenye umri kuanzia miaka makumi mbili na zaidi, mutawaweka katika hesabu ya majeshi yao. Kiongozi mumoja wa jamaa kutoka kila kabila atakusaidia kufanya hesabu. Hao viongozi waliochaguliwa kati ya watu wa Israeli walikuwa vilevile viongozi wa jeshi. Basi, Musa na Haruni wakawatwaa watu hao waliotajwa. Na katika siku ya kwanza ya mwezi wa pili, wakakusanya Waisraeli wote. Waliandika majina ya wote wenye umri wa miaka makumi mbili na zaidi, kulingana na jamaa zao na ukoo zao, kama vile Yawe alivyomwamuru Musa. Musa akawahesabu watu hawa kule katika jangwa la Sinai. Hao ndio watu waliokuwa wamehesabiwa ambao Musa na Haruni waliwahesabu wakisaidiwa na wale viongozi kumi na wawili wa Israeli, kila kiongozi akisimamia ukoo wake. Hivyo jumla ya wanaume wote wa Israeli wenye umri kuanzia miaka makumi mbili na zaidi, waliofaa kuingia katika jeshi katika inchi ya Israeli, ilikuwa watu elfu mia sita na tatu na mia tano makumi tano. Lakini Walawi hawakuhesabiwa pamoja na yale makabila mengine, kwa sababu Yawe alimwambia Musa: Usifanye hesabu ya kabila la Lawi pamoja na ile ya watu wa Israeli. Utawachagua wakuwe waangalizi wa hema la kuchunga vibao vya agano, vyombo vyake vyote na kila kitu kinachokuwa ndani yake; watakuwa wakilibeba pamoja na vyombo vyake vyote. Watatumika mule ndani na watapiga kambi yao kwa kulizunguka. Tena wakati wa hema kuongolewa, Walawi ndio watakaoliongoa. Na wakati wa hema kusimikwa, Walawi ndio watakaolisimamisha. Kama mutu ambaye si Mulawi analikaribia, atauawa. Waisraeli wengine wote watapiga kambi zao makundi makundi, kila mutu katika kundi lake na chini ya bendera yake. Lakini Walawi watapiga kambi zao kuzunguka hema la kuchunga vibao vya agano kusudi walilinde na kasirani yangu isiwake juu ya Waisraeli. Kwa hiyo Waisraeli wakafanya kama vile Yawe alivyomwamuru Musa. Yawe akawapa Musa na Haruni, maagizo haya: Waisraeli watapiga kambi zao, kila mumoja akikaa pahali penye bendera yake, penye vitambulisho vya ukoo wake. Watapiga kambi zao kuzunguka na kuelekea hema la mukutano. Wale watakaopiga kambi upande wa mashariki watakuwa kikundi cha watu wanaokuwa chini ya bendera ya Yuda na kiongozi wao atakuwa Nasoni mwana wa Aminadabu. Jeshi lake kulingana na hesabu ni wanaume elfu makumi saba na ine na mia sita. Wale watakaofuata kupiga kambi nyuma ya watu wa Yuda watakuwa kabila la Isakari. Kiongozi wao atakuwa Netaneli mwana wa Suari. Jeshi lake kulingana na hesabu ni wanaume elfu makumi tano na ine na mia ine. Kisha kabila la Zebuluni, kiongozi wao akiwa Eliabu mwana wa Heloni, jeshi lake kulingana na hesabu ni wanaume elfu makumi tano na saba na mia ine. Jumla yote ya watu watakaokuwa katika kambi ya Yuda kulingana na jeshi lake ni watu elfu mia moja makumi nane na sita na mia ine. Hao ndio watakaotangulia kusafiri. Kwa upande wa kusini, wale wanaokuwa chini ya bendera ya kundi la Rubeni kulingana na jeshi lake, kiongozi wao akiwa Elisuri mwana wa Sedeuri, jeshi lake kulingana na hesabu ni wanaume elfu makumi ine na sita na mia tano. Kisha wale watakaopiga kambi kando ya watu wa Rubeni watakuwa ni watu wa kabila la Simeoni, kiongozi wao akiwa Selumieli mwana wa Suri-Sadai, jeshi lake kulingana na hesabu ni wanaume elfu makumi tano na tisa na mia tatu. Halafu kabila la Gadi, kiongozi wao akiwa Eliasafu mwana wa Reueli, jeshi lake kulingana na hesabu ni wanaume elfu makumi ine na tano mia sita na makumi tano. Jumla ya wanaume watakaokuwa katika kambi ya Rubeni kulingana na jeshi lake ni watu elfu mia moja makumi tano na moja mia ine na makumi tano. Hawa ndio watakaokuwa katika kundi la pili. Halafu, kambi ya kabila la Walawi likiwa katikati ya kambi zote nao wakibeba hilo hema la mukutano wataondoka; kila kundi likisafiri kwa kufuata nafasi yake kwa bendera. Kwa upande wa magaribi, wale wanaokuwa chini ya bendera ya kundi la Efuraimu watapiga kambi kulingana na jeshi lake kiongozi wao akiwa Elisama mwana wa Amihudi, jeshi lake kulingana na hesabu ni wanaume elfu makumi tatu na mbili na mia mbili. Mara tu nyuma ya Waefuraimu litafuata kabila la Manase: kiongozi wake akiwa Gamalieli mwana wa Pedasuri, jeshi lake kulingana na hesabu litakuwa watu elfu makumi tatu na mbili na mia mbili. Kisha kabila la Benjamina: kiongozi wake ni Abidani, mwana wa Gideoni, jeshi lake kulingana na hesabu ni wanaume elfu makumi tatu na tano na mia ine. Jumla ya watu waliokuwa katika kambi ya Efuraimu kulingana na jeshi lake ni watu elfu mia moja na nane na mia moja. Hawa ndio watakaokuwa katika kundi la tatu. Kwa upande wa kaskazini, watapiga kambi katika jeshi lake wale wanaokuwa chini ya bendera ya Dani, kiongozi wao atakuwa Ahiezeri, mwana wa Amishadai, jeshi lake kulingana na hesabu litakuwa na watu elfu makumi sita na mbili na mia saba. Kisha wale watakaopiga kambi nyuma yao watakuwa watu wa kabila la Aseri, kiongozi wao akiwa Pagieli mwana wa Okrani, jeshi lake kulingana na hesabu litakuwa na watu elfu makumi ine na moja na mia tano. Kisha watu wa kabila la Nafutali, kiongozi wake akiwa Ahira mwana wa Enani, jeshi lake kulingana na hesabu, ni wanaume elfu makumi tano na tatu na mia ine. Jumla ya watu waliokuwa katika kambi ya Dani kulingana na jeshi lake ni watu elfu mia makumi tano na saba na mia sita. Hawa ndio watakaokuwa katika kundi la mwisho nyuma ya bendera zao. Hao ndio Waisraeli waliohesabiwa kulingana na ukoo zao, katika kambi na majeshi yao, wote walikuwa elfu mia sita na tatu na mia tano makumi tano. Lakini Walawi hawakuhesabiwa kati ya watu wa Israeli kama vile Yawe alivyomwamuru Musa. Hivi ndivyo, Waisraeli walivyofanya kila kitu kama vile Yawe alivyomwamuru Musa. Wakapiga kambi zao, kufuata bendera zao na wakasafiri kila mumoja akiandamana na jamaa yake kwa kufuata ukoo wake. Hawa ndio wazao wa Haruni na Musa wakati Yawe alipozungumuza na Musa kwenye mulima Sinai. Haya ndiyo majina ya wana wa Haruni: Nadabu, muzaliwa wake wa kwanza, Abihu, Eleazari na Itamari. Hawa walitakaswa kwa kupakwa mafuta wakuwe makuhani. Lakini Nadabu na Abihu walikufa mbele ya Yawe, wakati walipomutolea Yawe moto usiokuwa mutakatifu katika jangwa la Sinai. Wao hawakukuwa na watoto. Kwa hiyo Eleazari na Itamari wakatumika kama vile makuhani chini ya uongozi wa baba yao Haruni. Yawe akamwambia Musa: Uwalete karibu watu wa kabila la Lawi, uwaweke mbele ya kuhani Haruni wapate kumutumikia. Watafanya kazi kwa pahali pake na pa Waisraeli wote pamoja kwenye hema la mukutano wanapotumika pale. Watatunza vyombo vyote vya hema la mukutano na kuwasaidia Waisraeli wanapofanya kazi zao kwenye hema takatifu. Utamupatia Haruni Walawi na wazao wake makuhani; hao wametolewa kwake kabisa kati ya Waisraeli. Utachagua Haruni na wana wake kusudi waweze kutimiza kazi zao za ukuhani; lakini kama mutu yeyote mwingine akikaribia, atauawa. Yawe akaendelea kumwambia Musa: Sasa nimechagua Walawi kati ya Waisraeli wote, pahali pa kila muzaliwa wa kwanza mwanaume anayefungua tumbo la mama yake katika kila jamaa ya Israeli. Walawi ni wangu, maana kila muzaliwa wa kwanza katika Israeli ni wangu. Wakati nilipowaua wazaliwa wa kwanza wote wa Wamisri nilijitakasia kila muzaliwa wa kwanza katika Israeli; kila muzaliwa wa kwanza wa mwanadamu hata wa nyama; wao watakuwa wangu. Mimi ni Yawe. Yawe akamwambia Musa katika jangwa la Sinai: Uwahesabu wana wa Walawi wote kulingana na ukoo zao na jamaa zao, kila mwanaume kuanzia watoto wenye umri wa mwezi mumoja na zaidi. Basi, Musa akawahesabu kufuatana na neno la Yawe, kama vile alivyomwamuru. Hawa ndio waliokuwa wana wa Lawi: Gersoni, Kohati na Merari. Na haya ndiyo majina ya wana wa Gersoni kwa kufuata jamaa zao: Libuni na Simei. Wana wa Kohati kwa kufuata jamaa zao: Amuramu, Isihari, Hebroni na Uzieli. Wana wa Merari kwa kufuata jamaa zao: Mali na Musi. Hizi zilikuwa jamaa za Walawi kulingana na ukoo zao. Jamaa za Walibuni na Wasimei zilitokana na Gersoni; hizi ndizo zilizokuwa jamaa za Wagersoni. Hesabu yao kwa kadiri ya hesabu ya wanaume wote kuanzia waliokuwa na mwezi mumoja na zaidi ni elfu saba na mia tano. Ilipasa kwa jamaa za Wagersoni kupiga kambi yao upande wa magaribi, nyuma ya hema takatifu naye Eliasafu mwana wa Laeli akiwa mukubwa wa ukoo wa Wagersoni. Kazi ya wana wa Gersoni ilikuwa kutunza hema takatifu, hema pamoja na kifuniko chake, pazia la mulango wa hema la mukutano, mapazia ya upango unaokuwa kati ya hema takatifu na mazabahu, na pazia la mulango wa upango, na kamba zake. Kazi zote zilizoelekea vitu hivi zilikuwa zao. Jamaa za Waamuramu, Waisari, Wahebroni na Wauzieli zilitokana na Kohati; hizi ndizo zilizokuwa jamaa za Wakohati. Kadiri ya hesabu ya wanaume wote kuanzia wenye umri wa mwezi mumoja na zaidi ilikuwa elfu nane na mia sita, waliotumika katika Pahali Patakatifu. Jamaa za wana wa Kohati watapiga kambi yao upande wa kusini wa hema takatifu, naye Elisafani, akiwa mukubwa wa ukoo huo wa jamaa za Wakohati. Wao walioshugulika na kazi ya kutunza Sanduku la Agano, meza, kinara cha taa, mazabahu, vyombo makuhani wanavyotumia hema takatifu na pazia; kazi zote zilizoelekea vitu hivi zilikuwa zao. Naye Eleazari mwana wa kuhani Haruni aliwekwa kuwa mukubwa wa wakubwa wa Walawi, na musimamizi wa watumishi wote wa Pahali Patakatifu. Jamaa za Wamali na Wamusi zilitokana na Merari; hizi ndizo jamaa za Merari. Hesabu yao kadiri ya hesabu ya wanaume wote kuanzia wenye umri wa mwezi mumoja na zaidi ilikuwa watu elfu sita na mia mbili. Mukubwa wa ukoo wa jamaa za Merari alikuwa Surieli mwana wa Abihaili; hawa watapiga kambi yao upande wa kaskazini wa hema takatifu. Wao walipewa kazi ya kutunza mbao za hema takatifu, miti yake, nguzo, vitako na vifaa vyote vya kushikilia hema; kazi zote zilizoelekea vitu hivi zilikuwa juu yao. Vielvile walihitajika kutunza nguzo za upango zilizouzunguka na vitako vyake, misumari na kamba zake. Musa na Haruni na wana wao watapiga kambi yao mbele ya hema takatifu upande wa mashariki, ni kusema mbele ya hema la mukutano kuelekea upande linakotokea jua. Kazi yao itakuwa kutumika kwenye Pahali Patakatifu kwa jambo lolote lililohitajika kufanyika kwa ajili ya Waisraeli. Mutu mwingine yeyote aliyesogea karibu alipaswa kuuawa. Hesabu ya Walawi kulingana na jamaa zao, wanaume wote kuanzia watoto wenye umri wa mwezi mumoja na zaidi ambao Musa na Haruni waliwahesabu kwa amri ya Yawe, ilikuwa watu elfu makumi mbili na mbili. Kisha Yawe akamwambia Musa: Uwahesabu kwa majina wazaliwa wa kwanza wanaume wote wa Waisraeli kuanzia wenye umri wa mwezi mumoja na zaidi. Nawe utatenga Walawi kwa ajili yangu mimi Yawe; vilevile utatenga kwa ajili yangu mifugo yote ya Walawi pahali pa wazaliwa wa kwanza wa ngombe za watu wa Israeli. Basi, Musa akawahesabu wazaliwa wa kwanza wote wa watu wa Israeli kama vile Yawe alivyomwamuru. Wote wazaliwa wa kwanza wanaume kadiri ya hesabu ya majina, kuanzia wenye umri wa mwezi mumoja na zaidi, kufuata jinsi walivyohesabiwa, walikuwa elfu makumi mbili na mbili mia mbili makumi saba na tatu. Yawe akamwambia Musa: Sasa, utenge Walawi wote kuwa wangu pahali pa wazaliwa wa kwanza wa Waisraeli. Vilevile, utenge ngombe wa Walawi wote pahali pa wazaliwa wa kwanza wa ngombe wa Waisraeli. Mimi ni Yawe. Kwa ajili ya malipo ya wazaliwa wa kwanza wanaume wa watu wa Israeli mia mbili makumi saba na watatu, wanaozidi hesabu ya wanaume Walawi, utapokea kwa kila mwanaume feza shekeli tano, kulingana na kipimo cha Pahali Patakatifu, ambayo ni sawa na gera makumi mbili, na feza hizo kwa ajili ya malipo ya hao waliozidi hesabu yao utamupa Haruni na wana wake. Musa akatii, akatwaa feza hizo za malipo ya hao waliozidi hesabu ya waliolipiwa na Walawi; akapokea kutoka wazaliwa wa kwanza wa Waisraeli feza kiasi cha shekeli elfu moja mia tatu makumi sita na tano, kulingana na kipimo cha Pahali Patakatifu, akawapa Haruni na wana wake feza hizo za malipo sawa na neno la Yawe, kama vile alivyomwamuru. Yawe akamwambia Musa na Haruni: Uhesabu watu wa ukoo wa Kohati, toka katika ukoo za Lawi, kufuatana na jamaa zao na ukoo zao; utahesabu wanaume wote wenye umri kati ya miaka makumi tatu na makumi tano wanaofaa kujiunga na kazi ya hema la mukutano. Hii ndiyo itakayokuwa kazi ya wana wa Kohati, kuelekea vitu vitakatifu kabisa. Wakati wa kuvunja kambi, Haruni na wana wake wataingia katika hema, na kushusha pazia linalokuwa mbele ya Sanduku la Agano, kisha walifunike kwa pazia hilo. Juu yake wataweka kifuniko cha ngozi laini ya mbuzi, kisha watatandaza juu yake kitambaa cha rangi ya samawi tupu. Halafu wataingiza miti ya kulibebea sanduku hilo. Juu ya meza ya kutolea mikate inayowekwa mbele ya Yawe watatandaza kitambaa cha rangi ya samawi na juu yake wataweka sahani, visahani vya ubani, bakuli na bilauri, kwa ajili ya kutolea sadaka za kinywaji. Siku zote kutakuwa mukate juu ya meza. Kisha, watavifunika vyombo hivi vyote kwa kitambaa chekundu, na juu yake wataweka kifuniko cha ngozi laini ya mbuzi. Halafu wataingiza miti yake ya kulibebea. Watatwaa kitambaa cha rangi ya samawi ambacho watafunikia kinara cha taa na taa zake, makasi zake, sinia zake na vyombo vyote vinavyotumiwa kukiwekea mafuta. Watakiweka pamoja na vyombo vyake vyote ndani ya ngozi laini ya mbuzi na kukiweka juu ya miti ya kubebea. Halafu watatandaza kitambaa cha rangi ya samawi juu ya mazabahu ya zahabu na kuifunika kwa ngozi laini ya mbuzi. Halafu wataingiza miti yake ya kuibebea. Watatwaa vyombo vyote vinavyotumika katika Pahali Patakatifu, watavifunga kwa kitambaa cha rangi ya samawi na kuvifunika kwa ngozi laini ya mbuzi, kisha wataviweka juu ya miti yake ya kubebea. Wataondoa majivu juu ya mazabahu na juu yake watatandaza kitambaa cha rangi ya zambarau. Juu yake wataweka vyombo vyote vinavyotumika katika ibada kwenye mazabahu: vyetezo, makanya, miiko na mabakuli. Kisha, juu yake watatandaza kifuniko cha ngozi laini ya mbuzi na kuiingiza miti yake ya kulibebea. Kisha Haruni na wana wake kufunika Pahali Patakatifu pamoja na vyombo na vifaa vyake vyote, wakiwa tayari kuanza safari, watu wa ukoo wa Kohati watakuja na kuvibeba. Lakini wao, hawaruhusiwi kabisa kugusa vyombo hivyo vitakatifu, kusudi wasikufe. Hiyo ndiyo kazi ya ukoo wa Kohati kila wakati hema la mukutano linapohamishwa. Eleazari mwana wa kuhani Haruni atatunza mafuta ya taa, ubani wa kufukiza, sadaka za vyakula za kila siku, mafuta ya kupakaa kwa kutakasa na kila kitu kilichotakaswa katika hema hilo. Kisha Yawe akawaambia Musa na Haruni: Musiache ukoo wa jamaa za Kohati kati ya Walawi uangamizwe. Basi, kwa kuwaepusha wasipate kuuawa kwa kukaribia vyombo hivyo vitakatifu sana utafanya hivi: Haruni na wana wake wataingia na kumupangia kila mumoja wao mapaswa yake na kazi yake. Lakini wazao wa Kohati hawataingia kwa kutazama vitu hivyo vitakatifu sana wakifanya hivyo watakufa. Yawe akamwambia Musa: Uhesabu watu wa ukoo wa Gersoni kufuatana na jamaa na ukoo zao; utawahesabu wanaume wote wenye umri kati ya miaka makumi tatu na makumi tano wanaofaa kujiunga na kazi ya hema la mukutano. Utumishi wao utakuwa huu: watabeba mapazia ya hema takatifu na hema la mukutano pamoja na kifuniko chake, kifuniko cha ngozi laini ya mbuzi kinachokuwa juu yake, pazia la mulango, mapazia na kamba za upango unaokuwa kandokando ya hema na mazabahu, mapazia ya mulango wa kiwanja, na vifaa vyote vinavyotumika pamoja na vitu hivi. Wao watashugulika na mambo yote yanayoelekea vitu hivi. Haruni na wana wake makuhani ndio watakaoamrisha kazi zote za Wagersoni juu ya vitu watakavyobeba na kazi watakazofanya. Utawapangia vitu vyote vile ambavyo wanapaswa kubeba. Hii ndiyo kazi ya jamaa za Gersoni kwenye hema la mukutano; watafanya kazi chini ya uongozi wa Itamari mwana wa kuhani Haruni. Vilevile, utawahesabu wana wa Merari, kufuatana na jamaa zao na ukoo zao. Utawahesabu wanaume wote wenye umri kati ya miaka makumi tatu na makumi tano, wanaofaa kujiunga kwa kazi ya hema la mukutano. Wao watakuwa na kazi ya kubeba mbao, miti, nguzo na misingi ya hema la mukutano. Vilevile watabeba nguzo za upango za kuzunguka pande zote, viikalio, misumari na kamba pamoja na vifaa vyake vyote na vyombo vyake vingine vyote. Nawe utawapangia kufuatana na majina yao vitu watakavyopaswa kubeba. Hii ndiyo itakayokuwa kazi ya wana wa ukoo wa Merari katika utumishi wao wote ndani ya hema la mukutano, chini ya uongozi wa Itamari mwana wa kuhani Haruni. Basi, Musa, Haruni na viongozi wa Waisraeli wakafanya hesabu ya watu wa ukoo wa Kohati, kufuatana na jamaa zao, wakawahesabu watu wote wenye umri kati ya miaka makumi tatu na makumi tano, kila mutu aliyefaa kuingia katika kazi ya hema la mukutano. Hesabu yao kufuatana na jamaa zao ilikuwa watu elfu mbili mia saba na makumi tano. Hii ndiyo hesabu ya watu wa jamaa ya Wakohati, ambao walitumika katika hema la mukutano, ambao Musa na Haruni wakawahesabu kama vile Yawe alivyomwamuru Musa. Hesabu ya watu wa ukoo wa Gersoni kufuatana na jamaa zao, wenye umri kati ya miaka makumi tatu na makumi tano, waliofaa kutumika katika hema la mukutano, ilikuwa watu elfu mbili mia sita na makumi tatu. Hii ndiyo iliyokuwa hesabu ya watu wa jamaa za wana wa Gersoni wote waliotumika katika hema la mukutano, ambao Musa na Haruni waliwahesabu kama vile Yawe alivyowaamuru. Hesabu ya watu wa ukoo wa Merari kufuatana na jamaa zao na nyumba zao, wenye umri kati ya miaka makumi tatu na makumi tano waliofaa kutumika katika hema la mukutano, ilikuwa watu elfu tatu na mia mbili. Hii ndiyo hesabu ya watu wa ukoo wa Merari ambao Musa na Haruni waliwahesabu kama vile Yawe alivyomwamuru Musa. Hivyo, Walawi wote waliohesabiwa na Musa, Haruni na viongozi wa watu, kwa kufuata jamaa zao na ukoo zao, wenye umri kati ya miaka makumi tatu na makumi tano, na ambao walifaa kwa kazi na ubebaji katika hema la mukutano, kwa jumla walikuwa watu elfu nane na mia tano na makumi nane. Kila mumoja alipewa kazi yake ya kufanya juu ya kubeba hema la mukutano, kama vile Yawe alivyomwamuru Musa. Yawe akamwambia Musa: Uwaamuru Waisraeli wamutoe inje ya kambi kila mutu mwenye ukoma, kila mutu anayetokwa usaha, na kila anayekuwa muchafu kwa kugusa maiti. Mutawatoa inje ya kambi watu wote hawa, wanaume na wanawake, kusudi wasichafue kambi yangu ninamokaa. Waisraeli wakafanya hivyo, wakawafukuza inje ya kambi. Kama vile Yawe alivyomwambia Musa, ndivyo Waisraeli walivyofanya. Kisha Yawe akamwambia Musa: Uwaambie Waisraeli kwamba: Mutu yeyote, mwanaume au mwanamuke, akimukosea mwenzake, yeye anatenda zambi mbaya mbele ya Yawe. Anapaswa kutubu zambi yake aliyotenda; na atatoa malipo kamilifu kwa kosa lake, akiongeza asilimia makumi mbili ya malipo hayo; atatoa malipo hayo kwa yule aliyemukosea. Lakini ikiwa mutu huyo amekufa na hana ndugu wa karibu ambaye anaweza kupokea malipo hayo, basi, malipo ya kosa yatatolewa kwa Yawe kwa ajili ya makuhani; malipo haya ni pamoja na kondoo dume wa upatanisho ambaye atatumiwa kwa kumufanyia upatanisho kwa ajili ya zambi yake. Kila sadaka ya matoleo yote matakatifu ya Waisraeli watakayomuletea kuhani, itakuwa yake. Na kila kitu kitakatifu cha mutu kitakuwa cha kuhani; kitu chochote mutu anachomutolea kuhani kitakuwa chake. Yawe akamwambia Musa: Uwaambie Waisraeli: Kama muke wa mutu yeyote amepotoka na kukosa uaminifu kwa mume wake, akilala na mutu mwingine bila mume wake au mutu mwingine yeyote kujua; amejichafua ingawa hakuna mutu aliyeshuhudia kitendo chake kwa sababu hakukamatwa. Lakini, mume wake akiingiwa na shaka na kuwa na wivu juu ya muke wake aliyejichafua; au kama amekuwa na wivu juu ya muke wake ingawa muke wake hakujichafua, basi wote wawili watakwenda kwa kuhani na kupeleka sadaka inayotakiwa, ni kusema sehemu ya kumi ya unga wa shayiri; lakini bila kuitia mafuta au ubani, kwa sababu ni sadaka ya vyakula ya mume anayekuwa na wivu kwa muke wake, kwa ukumbusho wa kosa. Kuhani atamupeleka huyo mwanamuke karibu, na kumusimamisha mbele ya Yawe. Kisha, atamimina maji matakatifu katika chombo cha udongo na atatwaa vumbi inayokuwa chini ndani ya hema takatifu na kuitia katika maji hayo kwa kuyafanya machungu. Kuhani atamuweka mbele ya Yawe na kumufunua nywele na kumupa sadaka hiyo ya vyakula inayotolewa kwa sababu ya wivu wa mume wake. Kuhani mwenyewe atashikilia kile chombo chenye maji machungu yanayoleta laana. Halafu kuhani atamwapisha mwanamuke huyo akisema: Ikiwa haukulala na mwanaume mwingine na kujichafua wakati uko chini ya mamlaka ya mume wako, basi, hautapatwa na laana inayoletwa na maji haya machungu. Lakini kama umepotoka wakati uko chini ya mamlaka ya mume wako, na kujichafua kwa kulala na mwanaume mwingine asiyekuwa mume wako, Yawe akuazibu hata ukuwe laana na kiapo kati ya watu wako, ukuwe tasa na tumbo lako livimbe. Maji haya yanayoleta laana yaingie ndani ya tumbo lako na kukufanya tasa na tumbo lako livimbe. Naye mwanamuke ataitikia: Amina! Amina! Kisha kuhani ataandika laana hizi katika kitabu na kuzisafisha katika maji machungu. Atamukunywesha mwanamuke hayo maji machungu yanayaleta laana nayo yataingia ndani yake na kumuletea maumivu makali. Kisha kuhani atatwaa ile sadaka ya vyakula ya wivu katika mikono ya mwanamuke huyo na kuitikisa mbele ya Yawe, na kuipeleka juu ya mazabahu. Halafu, atatwaa mukono mumoja wa sadaka hiyo ya vyakula kwa ukumbusho na kuiteketeza juu ya mazabahu. Kisha atamukunywesha mwanamuke maji hayo. Akisha kunywa, kama amejichafua na hakukuwa mwaminifu kwa mume wake maji hayo yanayoleta laana yataingia ndani ya matumbotumbo yake na kuwa machungu, na tumbo lake litavimba naye atakuwa tasa. Mwanamuke huyo atakuwa laana kati ya watu wake. Lakini kama mwanamuke huyo hajajichafua na hana kosa, basi hatapatwa na hasara na ataweza kupata watoto. Basi, hii ndiyo sheria kuelekea maneno ya wivu kama mwanamuke akiwa chini ya mamlaka ya mume wake, anapotoka na kujichafua, au wakati mwanaume anaposhikwa na wivu na kuwa na mashaka na muke wake. Atamusimamisha mwanamuke huyo mbele ya Yawe, na kuhani atatimiza masharti yote ya sheria hii. Mume wake hatakuwa na kosa lolote, lakini mwanamuke atabeba lazima ya uovu wake. Yawe akamwambia Musa: Uwape Waisraeli maagizo haya: Ikiwa mwanaume au mwanamuke atafanya kiapo kuwa munaziri, ni kusema kujitenga kwa ajili ya Yawe, basi, asikunywe divai au kileo, asikunywe siki ya divai au ya namna nyingine, asikunywe maji ya zabibu wala kula zabibu zilizoiva au kavu. Muda wote atakaokuwa munaziri asikule kitu chochote kinachotokana na muzabibu, tangu kokwa hata maganda yake. Siku zote za kiapo chake cha kujitenga, hatanyoa nywele zake. Mpaka muda wa kiapo chake cha kujitakasa kwa Yawe utakapomalizika, atakuwa mutakatifu, ataacha nywele zake zikuwe ndefu. Siku zote atakazokuwa amejitakasa kwa Yawe, mutu huyo asikaribie maiti, hata kama ni ya baba, mama, ndugu au dada yake, kusudi asijichafue kwa maana amejitakasa kwa Yawe kwa kiapo. Muda wote atakaokuwa munaziri atakuwa mutakatifu kwa Yawe. Kama mutu anakufa kwa rafla karibu na munaziri na kuchafua nywele zake, huyu munaziri atanyoa kichwa chake wakati wa siku ya kutakaswa kwake; atakinyoa katika siku ya saba. Katika siku ya nane atapeleka hua wawili au vitoto viwili vya njiwa kwa kuhani kwenye mulango wa hema la mukutano. Kuhani atamutoa mumoja kuwa sadaka kwa ajili ya zambi na mwingine kuwa sadaka ya kuteketezwa, naye atamufanyia ibada ya upatanisho, kwa sababu alitenda zambi kwa sababu ya maiti. Siku hiyohiyo atatakasa kichwa chake na kujitakasa kwa Yawe kwa siku zake za kujitenga. Hizo siku za kwanza hazitahesabiwa kwa sababu nywele zake zilizokuwa zimetakaswa zimechafuka. Atatoa mwana-kondoo dume wa mwaka mumoja kuwa sadaka ya kosa. Hii ndiyo sheria ya munaziri wakati akisha kamilisha muda wake wa kujitakasa: Ataletwa kwenye mulango wa hema la mukutano, na kumutolea Yawe zawadi zake: mwana-kondoo dume mumoja wa mwaka mumoja asiyekuwa na kilema kwa ajili ya sadaka ya kuteketezwa; mwana-kondoo dike mumoja wa mwaka mumoja asiyekuwa na kilema kwa ajili ya sadaka ya zambi; na kondoo dume mumoja asiyekuwa na kilema kwa ajili ya sadaka ya amani. Vilevile atatoa kikapu cha mikate isiyotiwa chachu: maandazi ya unga laini na mafuta, na mikate myembamba iliyopakwa mafuta pamoja na sadaka za vyakula na za kinywaji. Kuhani atamutolea Yawe vitu vyote hivi pamoja na sadaka yake ya zambi na sadaka yake ya kuteketezwa. Atamutolea Yawe huyo kondoo kama sadaka ya amani, atamutoa pamoja na kikapu cha mikate isiyotiwa chachu, sadaka ya vyakula na ya kinywaji. Hapo kwenye mulango wa hema la mukutano, munaziri huyo atanyoa nywele zake na kuzitia katika moto unaokuwa chini ya sadaka ya amani. Kisha kuhani atatwaa bega la yule kondoo dume likiwa limepikwa pamoja na andazi moja lililotiwa chachu kutoka kikapu na mikate myembamba vilevile isiyotiwa chachu na kumupa munaziri katika mikono akisha kumaliza kunyoa nywele zake alizokuwa nazo wakati wa kutakaswa. Halafu kuhani atavitikisa vitu hivyo kama sadaka ya kutikisa mbele ya Yawe; vyote hivi ni sehemu takatifu kwa kuhani, pamoja na kilali kilichotikiswa na paja lililotolewa kama sadaka. Nyuma ya hayo yote, munaziri anaweza kunywa divai. Hiyo ndiyo sheria inayoelekea munaziri anayeahidi kwa kiapo. Sadaka yake kwa Yawe ilingane na kiapo chake, zaidi ya kitu chochote kingine anachoweza kutoa; atafanya kulingana na kiapo alichoweka, kadiri ya sheria ya kujitakasa kwake. Yawe akamwambia Musa: Uwambie Haruni na wana wake kwamba hivi ndivyo mutakavyowabariki Waisraeli: Mutawaambia: Yawe awabariki na kuwalinda; Yawe awaangalie kwa wema, na kuwatendea mema; Yawe awaonyeshe wema wake na kuwapa amani. Ndivyo watakavyotamka jina langu juu ya Waisraeli, nami nitawabariki. Siku Musa alipomaliza kusimamisha hema takatifu, akalimiminia mafuta na kulitakasa pamoja na vyombo vyake vyote. Akamiminia mazabahu mafuta na kuitakasa pamoja na vyombo vyake vyote. Viongozi wa Israeli na wakubwa wa ukoo na viongozi wa makabila ambao walisimamia watu wale waliohesabiwa, wakamuletea Yawe matoleo yao: magari sita yaliyofunikwa na ngombe dume kumi na wawili, gari moja kwa kila viongozi wawili na ngombe dume mumoja kwa kila kiongozi. Kisha kuvitoa mbele ya hema takatifu, Yawe akamwambia Musa: Pokea matoleo haya kusudi yatumiwe katika kazi itakayofanywa kwa ajili ya hema la mukutano, uwape Walawi, kila mumoja kwa kadiri ya kazi yake. Basi, Musa akatwaa magari na ngombe dume akawapa Walawi. Wagersoni wakapewa magari mawili na ngombe dume wane, kwa kadiri ya kazi yao, na Wamerari wakapewa magari mane na ngombe dume wanane kwa kuwasaidia katika kazi zao zote chini ya uongozi wa Itamari mwana wa kuhani Haruni. Lakini Musa hakuwapa Wakohati kitu chochote kwa sababu wao walikuwa na utumishi wa kutunza vitu vitakatifu ambavyo vilipaswa kubebwa juu ya mabega. Viongozi hao wakatoa sadaka kwa ajili ya kuitakasa mazabahu siku ile ilipopakwa mafuta; walitoa sadaka zao mbele ya mazabahu. Yawe akamwambia Musa: Kila siku kiongozi mumoja atatoa sadaka yake kwa ajili ya kutakasa mazabahu. Jumla ya matoleo ya sadaka za viongozi wa Israeli kwa ajili ya mazabahu siku ilipotakaswa ilikuwa: sahani za feza kumi na mbili, beseni za feza kumi na mbili, na visahani vya zahabu kumi na viwili. Kila sahani ya feza, ilikuwa yenye uzito wa kilo moja na nusu na kila kisahani kilikuwa chenye uzito wa grama mia nane. Hivyo vyombo vyote vilikuwa na uzito wa kilo makumi mbili na saba na grama mia sita kadiri ya vipimo vya hema takatifu. Vile visahani vya zahabu kumi na viwili vyenye kujaa ubani, kila kimoja kikiwa na uzito wa grama mia moja na kumi kadiri ya vipimo vya hema takatifu vilikuwa na jumla ya uzito wa kilo moja na grama mia tatu makumi mbili. Jumla ya nyama wote wa sadaka ya kuteketezwa ilikuwa ngombe dume kumi na wawili, kondoo dume kumi na wawili, na wana-kondoo dume wa mwaka mumoja kumi na wawili, pamoja na sadaka ya vyakula na beberu kumi na wawili kwa ajili ya sadaka ya zambi, na kwa ajili ya sadaka ya amani, jumla ya nyama waliotolewa ilikuwa ngombe dume makumi mbili na wane, kondoo dume makumi sita, beberu makumi sita, na wana-kondoo dume wa mwaka mumoja makumi sita. Hiyo ndiyo iliyokuwa sadaka iliyotolewa kwa ajili ya mazabahu, kisha mazabahu hayo kupakwa mafuta. Wakati Musa alipoingia ndani ya hema la mukutano kwa kuongea na Yawe, akasikia sauti kutoka upande wa juu wa kiti cha rehema, kilichokuwa juu ya Sanduku la Agano, kutoka kati ya wale makerubi. Yawe akamwambia Musa: Umwambie Haruni kwamba wakati atakapoweka zile taa saba kwenye kinara, azipange kusudi ziangaze upande wa mbele wa kinara hicho. Haruni akatii maagizo hayo, akaweka taa hizo kusudi ziangaze upande wa mbele wa kinara, kama vile Yawe alivyomwamuru Musa. Toka sehemu za juu mpaka chini kinara hicho cha taa kilikuwa kimetengenezwa kwa ufundi mukubwa kwa zahabu iliyofuliwa kufuatana na mufano ambao Yawe alikuwa amemwonyesha Musa. Tena Yawe akamwambia Musa: Uwatenge Walawi kutoka Waisraeli na kuwatakasa. Hivi ndivyo utakavyowatakasa: uwanyunyizie maji ya utakaso kisha uwaambie wajinyoe mwili muzima, wafue nguo zao na kujitakasa. Kisha watatwaa mwana-ngombe dume mumoja pamoja na sadaka yake ya vyakula, ni kusema unga laini uliochanganywa na mafuta; nawe utatwaa mwana-ngombe dume wingine kwa ajili ya zambi. Kisha utawakusanya watu wote wa Israeli na kuwaleta Walawi mbele ya hema la mukutano. Utakapowaleta Walawi mbele yangu, Waisraeli watawawekea Walawi mikono. Halafu Haruni atawaweka hao mbele yangu kama sadaka ya kutikiswa kutoka kwa Waisraeli wanitumikie. Kisha Walawi wataweka mikono yao juu ya vichwa vya ngombe dume hao; mumoja wao utamutoa kuwa sadaka kwa ajili ya zambi, na huyo mwingine utamutoa kuwa sadaka ya kuteketezwa inayotolewa kwangu, kwa kuwafanyia Walawi upatanisho. Kisha utawasimamisha Walawi mbele ya Haruni na wana wake na kuwaweka mbele yangu kama vile sadaka ya kutikiswa. Hivi ndivyo utakavyowatenga Walawi kati ya Waisraeli wengine kusudi wakuwe wangu. Kisha kuwatakasa Walawi na kuwatoa kama vile sadaka ya kutikiswa wataingia kwa kutumika katika hema la mukutano. Hao wametolewa wakuwe wangu kabisa, pahali pa wazaliwa wa kwanza wa Waisraeli. Maana wazaliwa wote wa kwanza kati ya Waisraeli ni wangu, wanadamu na nyama; maana niliwatakasa kwa ajili yangu siku nilipowaua wazaliwa wote wa kwanza katika inchi ya Misri. Sasa ninawatwaa Walawi pahali pa wazaliwa wa kwanza wa Waisraeli, na nimewatoa kwa Haruni na wana wake, kama vile zawadi kutoka kwa Waisraeli, kusudi wafanye kazi katika hema la mukutano kwa ajili ya Waisraeli na kuwafanyia upatanisho kusudi kusitokee pigo kati ya Waisraeli wakikaribia Pahali Patakatifu. Kwa hiyo Musa, Haruni na Waisraeli wote pamoja wakatakasa Walawi, kama vile Yawe alivyomwamuru Musa. Walawi wakajitakasa zambi na kufua nguo zao, naye Haruni akawatoa kama vile sadaka ya kutikiswa mbele ya Yawe. Vilevile, Haruni akafanya upatanisho kwa ajili yao kwa kuwatakasa. Kisha hayo Walawi wakaingia na kufanya kazi yao katika hema la mukutano chini ya usimamizi wa Haruni na wana wake, kama vile Yawe alivyomwamuru Musa. Yawe akamwambia Musa: Kila Mulawi mwenye umri wa miaka makumi mbili na mitano na zaidi, atatumika katika hema la mukutano. Na tangu umri wa miaka makumi tano ataacha kazi; asitumike tena. Lakini, anaweza kuwasaidia Walawi wenzake wanapotumika katika hema, lakini haruhusiwi kufanya kazi yoyote peke yake. Ndivyo utakavyowapangia Walawi kazi. Kisha katika mwezi wa kwanza wa mwaka wa pili nyuma ya Waisraeli kutoka Misri, Yawe akasema na Musa katika jangwa la Sinai. Akamwambia: Waisraeli washike sikukuu ya Pasaka kwa wakati uliopangwa. Hii itakuwa siku ya kumi na ine ya mwezi huu, wakati wa magaribi watafanya hivyo kufuatana na masharti na maagizo yake yote. Kwa hiyo, Musa akawaambia watu kwamba wanapaswa kushika sikukuu ya Pasaka. Basi, wakafanya Pasaka magaribi, siku ya kumi na ine ya mwezi wa kwanza, katika jangwa la Sinai. Waisraeli wakafanya yote kama vile Yawe alivyomwamuru Musa. Lakini, watu wamoja waliokuwa pale walikuwa hawawezi kushiriki sikukuu hiyo ya Pasaka kwa sababu walikuwa wamegusa maiti, wakakuwa wachafu. Hao waliwaendea Musa na Haruni, wakawaambia: Sisi tuko wachafu kwa sababu tumegusa maiti, lakini kwa nini tukatazwe kumutolea Yawe sadaka zake kwa wakati uliopangwa pamoja na Waisraeli wengine? Musa akawajibu: Mungojee mpaka pale nitakapopata maagizo juu yenu kutoka kwa Yawe. Naye Yawe akamwambia Musa: Mumoja wenu au mumoja wa wazao wenu akiwa muchafu kwa sababu amegusa maiti au akiwa mbali katika safari, lakini akiwa anataka kunifanyizia sikukuu ya Pasaka, mutu kama huyo anaruhusiwa kufanya hivyo mwezi mumoja kisha, magaribi ya siku ya kumi na ine ya mwezi wa pili. Ataifanya kwa kula mikate isiyotiwa chachu na mboga chungu. Wasiache chakula chochote mpaka asubui, wala wasivunje hata mufupa mumoja wa nyama wa Pasaka. Watafanya sikukuu hii ya Pasaka kulingana na sharti lake lote. Lakini mutu yeyote ambaye ni safi au hayuko katika safari asipofanya sikukuu ya Pasaka, atatengwa na watu wake kwa kuwa hakunitolea sadaka kwa wakati uliopangwa. Mutu huyo atabeba lazima ya zambi yake. Ikiwa kuna mugeni anayeishi pamoja nanyi na anapenda kufanya sikukuu ya Pasaka, mutu huyo sharti afanye hivyo kulingana na masharti na maagizo yote ya Pasaka. Kila mutu atafuata masharti yaleyale, akiwa mugeni au mwenyeji. Siku ambayo hema takatifu lilisimikwa, wingu likashuka na kufunika hema la kuchunga vibao vya agano. Wakati wa usiku wingu hilo lilionekana kama moto mpaka asubui. Hivi ndivyo ilivyokuwa kila siku; wingu lilifunika hema muchana, na usiku lilionekana kama moto. Kila mara wingu hilo lilipoinuliwa juu ya hema, Waisraeli walivunja kambi na kupiga kambi tena pahali wingu hilo lilipotua. Walisafiri kwa amri ya Yawe, na kupiga kambi tena kwa amri yake. Muda wote wingu hilo lilipokuwa juu ya hema, watu walikaa katika kambi hiyo. Hata kama wingu hilo lilikaa juu ya hema kwa muda wa siku nyingi, Waisraeli walimutii Yawe, nao hawakuondoka. Wakati mwingine wingu hilo lilikaa juu ya hema kwa muda wa siku chache tu. Kwa agizo la Yawe, Waisraeli walipiga kambi na ni kwa agizo la Yawe walisafiri. Wakati mwingine wingu lilikaa juu ya hema tangu magaribi mpaka asubui tu; na mara tu lilipoinuliwa, hao watu vilevile walifunga safari. Na ikiwa lilikaa juu ya hema muchana kutwa na usiku kucha, wao waliondoka tu wingu lilipoinuliwa. Ikiwa ni siku mbili, mwezi, mwaka au zaidi, muda wote wingu hilo lilipokuwa juu ya hema, Waisraeli hawakuhama; lakini lilipoinuliwa, nao vilevile walihama. Kwa agizo la Yawe walipiga kambi na kwa agizo la Yawe walisafiri. Walishika agizo la Yawe kama vile alivyotoa amri yake kwa njia ya Musa. Yawe akamwambia Musa: Tengeneza baragumu mbili kwa feza iliyofuliwa. Utatumia baragumu hizo wakati wa kuwaita watu na wakati wa kuvunja kambi. Baragumu zote mbili zikipigwa pamoja, watu wote watakusanyika karibu nawe mbele ya mulango wa hema la mukutano. Lakini kama ikipigwa baragumu moja tu, basi ni viongozi tu wa makabila ya Israeli watakaokusanyika karibu nawe. Alama hiyo ikitolewa kwa kupiga baragumu, wakaaji wa kambi za upande wa mashariki wataanza safari. Alama hiyo ikipigwa mara ya pili, wale wa kambi za upande wa kusini wataanza kuondoka. Alama hiyo ya baragumu itatolewa kila wakati wa kuanza safari. Lakini wakati wa kuwaita watu wakusanyike pamoja, baragumu zitapigwa kwa njia ya kawaida. Wazao wa Haruni, makuhani, ndio watakaopiga baragumu hizo. Utaratibu huo utakuwa sharti la kufuata siku zote katika vizazi vyenu vyote. Wakati wa vita katika inchi yenu juu ya waadui wanaowashambulia, mutatoa kitambulisho cha vita kwa kupiga baragumu hizi kusudi Yawe, Mungu wenu apate kuwakumbuka na kuwaokoa na waadui zenu. Vilevile katika siku zenu za furaha, kama vile sikukuu za mwandamo wa mwezi na sikukuu nyingine, mutapiga baragumu hizi wakati munapotoa sadaka zenu za kuteketezwa na sadaka zenu za amani. Hapo mimi Mungu wenu nitawakumbuka. Mimi ni Yawe, Mungu wenu. Katika siku ya makumi mbili ya mwezi wa pili, mwaka wa pili tangu watu wa Israeli walipoondoka Misri, wingu lililokuwa juu ya hema la kuchunga vibao vya agano likainuliwa, nao Waisraeli wakaanza safari yao kutoka jangwa la Sinai. Wingu hilo likapanda na kisha likatua katika jangwa la Parani. Kwa mara ya kwanza Waisraeli walifunga safari hiyo kwa amri ya Yawe kama ilivyotolewa na Musa. Wale waliokuwa chini ya bendera ya jeshi la kabila la Yuda, wakatangulia, kundi moja kisha lingine. Kiongozi wao alikuwa Nasoni mwana wa Aminadabu. Netaneli mwana wa Suari, alikuwa kiongozi wa jeshi la kabila la Isakari. Naye Eliabu mwana wa Heloni, alikuwa kiongozi wa jeshi la kabila la Zebuluni. Kisha, hema likashushwa, na watu wa ukoo wa Gersoni na wa Merari ambao walilibeba, walianza kuondoka. Halafu, watu waliokuwa chini ya bendera ya jeshi lililoongozwa na kabila la Rubeni, wakafuata kundi moja nyuma ya lingine. Kiongozi wao alikuwa Elisuri mwana wa Sedeuri. Selumieli mwana wa Suri-Shadai, aliongoza kabila la Simeoni. Naye Eliasafu mwana wa Deueli, aliongoza kabila la Gadi. Kisha walifuata watu wa ukoo wa Kohati, wakiwa wamebeba vyombo vitakatifu. Walipofika, hema lilikuwa limekwisha kusimikwa. Nyuma ya hao, wakafuata watu waliokuwa chini ya bendera ya jeshi lililoongozwa na kabila la Efuraimu, kundi moja nyuma ya lingine. Kiongozi wao alikuwa Elisama mwana wa Amihudi. Gamalieli mwana wa Pedasuri aliongoza kabila la Manase, naye Abidani mwana wa Gideoni, aliongoza kabila la Benjamina. Mwisho, wale waliokuwa chini ya bendera ya jeshi lililoongozwa na kabila la Dani, waliokuwa kama walinzi nyuma ya majeshi yote, wakasafiri, kundi moja nyuma ya lingine. Hawa waliongozwa na Ahiezeri mwana wa Amishadai. Pagieli mwana wa Okrani, aliongoza kabila la Aseri. Naye Ahira mwana wa Enani, aliongoza kabila la Nafutali. Huu basi, ndio utaratibu Waisraeli waliofuata kulingana na makundi yao, kila wakati walipovunja kambi na kuanza kusafiri tena. Musa akamwambia shemeki yake Hobabu mwana wa Reueli Mumidiani, baba mukwe wake: Sisi tunasafiri kwenda pahali ambapo Yawe amesema: Nitawapa ninyi pahali hapo. Basi, tuende pamoja, nasi tutakutendea vizuri maana Yawe ameahidi kutendea Waisraeli vizuri. Lakini Hobabu akajibu: Mimi sitakwenda nanyi; lakini nitarudi katika inchi yangu na kwa wandugu zangu. Musa akamwambia: Tafazali usituache, maana wewe unajua pahali tunapoweza kupiga kambi katika jangwa, na unaweza kuwa mwongozi wetu. Tena ukienda nasi chochote chema Yawe atakachotutendea, ndicho utakachotendewa nawe vilevile. Basi, watu wakasafiri toka Sinai, mulima wa Yawe, mwendo wa siku tatu. Sanduku la Agano la Yawe liliwatangulia mwendo wa siku tatu, kwa kuwatafutia pahali pa kupigia kambi. Kila mara waliposafiri kutoka kambi moja mpaka ingine, wingu la Yawe lilikuwa juu yao muchana. Kila wakati sanduku liliposafiri kwenda mbele, Musa alisema: Inuka, ee Yawe, uwatawanye waadui zako, na hao wanaokuchukia uwafanye wakimbie kutoka mbele yako. Na kila wakati liliposimama, Musa alisema: Uwarudilie, ee Yawe, hawa maelfu na maelfu ya Israeli. Watu wakaanza kunungunika mbele ya Yawe juu ya taabu zao. Yawe akasikia, na hasira yake ikawaka. Moto toka kwa Yawe ukawaka kati yao na kuchoma upande mumoja wa kambi. Watu wakamulilia Musa, naye akamwomba Yawe na moto huo ukazimika. Kwa hiyo, pahali pale pakaitwa Tabera, ni kusema “Kuchoma”, kwa sababu pale moto wa Yawe uliwaka kati ya watu. Kati ya Waisraeli kulikuwa kundi fulani lililoandamana nao ambalo lilikuwa na hamu kubwa ya kula nyama. Waisraeli wenyewe wakalia, wakisema: Heri kama tungeweza kupata nyama ya kula! Tunakumbuka, samaki tuliokula katika Misri bila malipo, maboga, matikiti, mboga, vitunguu na vitunguu sumu! Lakini sasa nguvu zimetuishia na hakuna chakula kingine isipokuwa hii mana tu! Mana ilikuwa kama mbegu ndogo zenye rangi ya kimanjano. Watu walizungukazunguka na kuikusanya, kisha waliisaga kwa mawe ya kusagia au waliitwanga katika vinu, halafu waliitokotesha ndani ya vyungu na kutengeneza maandazi. Onjo yake ilikuwa kama ya maandazi yaliyokaangwa kwa mafuta. (Umande ulipoanguka katika kambi wakati wa usiku, mana vilevile ilianguka pamoja na huo umande). Musa akasikia watu wakilia katika jamaa zote, kila mutu kwenye mulango wa hema lake. Basi, hasira ya Yawe ikawaka sana; naye Musa akachukizwa. Halafu Musa akamwambia Yawe: Kwa nini unanitendea vibaya mimi mutumishi wako? Mbona sikupata kukubaliwa mbele yako? Kwa nini umenibebesha muzigo wa kuwatunza watu hawa wote? Ni mimi ndiye niliyewazaa, hata ukaniambia niwabebe kwenye kifua changu kama mulezi anavyobeba mutoto muchanga, na kuwapeleka mpaka katika inchi uliyoapa kuwapa babu zao? Nitapata wapi nyama ya kuwakulisha watu hawa wote? Maana wanalia mbele yangu wakisema: Utupatie nyama tukule! Siwezi kuwatunza watu wote hawa peke yangu; kwa sababu ni muzigo muzito kwangu! Ikiwa hivi ndivyo utakavyonitendea, afazali uniue mara moja! Kama ninapata kukubaliwa mbele yako, usiniache kuendelea katika taabu yangu. Basi, Yawe akamwambia Musa: Uwakusanye wazee makumi saba wa Israeli, ambao wewe unajua wanaheshimiwa na kukubaliwa na watu kuwa viongozi, uwalete kwenye hema la mukutano, wasimame karibu nawe. Nitashuka kule na kuzungumuza nawe; nitatwaa sehemu ya roho niliyokupa, niwape watu hao. Nao watabeba muzigo wa kuwatunza watu hawa pamoja nawe, kusudi usibebe muzigo huo peke yako. Sasa uwaambie watu hivi: Mujitakase kwa ajili ya kesho; mutakula nyama. Yawe amesikia mukilia na kusema kwamba hakuna wa kuwapa nyama, na kwamba hali yenu ilikuwa nzuri zaidi mulipokuwa Misri. Sasa Yawe atawapa nyama, nanyi sherti mutaikula. Mutakula nyama si kwa muda wa siku moja tu, au mbili, au tano, au kumi au makumi mbili, lakini kwa muda wa mwezi muzima! Mutaikula mpaka iwatoke ndani ya pua, mpaka muichukie. Yote hayo ni kwa sababu mumemukataa Yawe anayekuwa hapahapa kati yenu, na kulia mbele yake mukisema: Kwa nini tulitoka Misri? Lakini Musa akamwambia Yawe: Hesabu ya watu ninaowaongoza hapa ni elfu mia sita wanaoenda kwa miguu, nawe unasema: Nitawapa nyama ya kuwatosha mwezi muzima! Kunaweza kuchinjwa kondoo na ngombe wa kuwatosheleza? Samaki wote bahari wavuliwe kwa ajili yao? Yawe akamujibu Musa: Uwezo wangu umepunguka? Utaona basi kama neno langu litakuwa la kweli kwako au hapana. Basi, Musa akaenda na kuwajulisha watu yale Yawe aliyosema. Kisha, akakusanya wazee makumi saba kutoka kati ya wazee viongozi nao akawaweka kandokando kuzunguka hema. Hapo, Yawe akashuka katika wingu na kuzungumuza naye. Halafu akatwaa sehemu ya roho aliyokuwa amemupa Musa, akawapa kila mumoja wa wale wazee makumi saba. Walipoingiwa na roho huyo, wazee hao wakaanza kutoa unabii, lakini hawakurudia kufanya hivyo. Wazee wawili kati ya wale makumi saba waliochaguliwa, Eldadi na Medadi, walikuwa wamebaki katika kambi wenzao walipokwenda kwenye hema. Roho iliwafikia humohumo ndani ya kambi, wakaanza kutoa unabii pahali walipokuwa. Kijana mumoja akatoka mbio na kumwambia Musa: Eldadi na Medadi wanatoa unabii ndani ya kambi. Hapo, Yoshua mwana wa Nuni, ambaye alikuwa musaidizi wa Musa tangu ujana wake, akamwambia Musa: Bwana wangu, uwakataze! Lakini Musa akamujibu: Unaona wivu kwa ajili yangu? Heri Yawe angewapa watu wake wote roho yake nao wapate kuwa manabii! Kisha Musa akarudi katika kambi pamoja na wale wazee makumi saba wa Israeli. Nyuma ya pale, Yawe akavumisha upepo kwa rafla, ukaleta kwale kutoka katika bahari na kuwafanya watue kando ya kambi, mwendo wa siku moja hivi kila upande kuzunguka kambi, wakalundikana chini karibu metre moja hivi kwenda juu. Basi, siku hiyo yote, usiku kucha, na siku iliyofuata watu walikusanya kwale; hakuna mutu aliyekusanya chini ya kilo elfu moja. Wakawaanika kila pahali kandokando ya kambi kwa kuwakausha. Kulikuwa kungali nyama kwa wingi na mbele watu hawajawamaliza kula, Yawe akawakasirikia watu, akawapiga watu kwa pigo kubwa sana. Kwa hiyo pahali pale pakapewa jina Kibroti-Hatawa, ni kusema “Makaburi ya Hamu”, kwa sababu huko ndiko walikozika watu waliokuwa na hamu ya kula nyama. Kutoka hapo Kibroti-Hatawa watu wakasafiri mpaka Haseroti, wakapiga kambi yao na kukaa kule. Kisha Miriamu na Haruni wakaanza kumusema Musa vibaya kwa sababu ya mwanamuke Mukushi aliyekuwa amemwoa. Wakasema: Basi, Yawe amezungumuza kwa kumwagiza Musa peke yake? Si amezungumuza nasi vilevile? Yawe akasikia maneno hayo. (Musa alikuwa mutu munyenyekevu kuliko watu wengine wote waliokuwa katika dunia.) Halafu kwa rafla, Yawe akawaambia Musa, Haruni na Miriamu: Mukuje katika hema la mukutano, ninyi watatu. Basi, wote watatu wakaenda kwenye hema la mukutano. Hapo Yawe akashuka katika nguzo ya wingu, akasimama kwenye mulango wa hema, akawaita Haruni na Miriamu. Wote wawili wakasogea mbele. Kisha Yawe akawaambia: Musikilize maneno yangu, kama kuna nabii kati yenu, mimi Yawe ninajifahamisha kwake katika maono na kuongea naye katika ndoto. Lakini juu ya mutumishi wangu Musa, hali ni tofauti kabisa. Yeye ana madaraka ya kuwatunza watu wangu wote. Mimi ninaongea naye kinywa kwa kinywa, waziwazi na si kwa kutumia mafumbo. Yeye ameliona umbo langu mimi Yawe. Kwa nini, basi, hamukuogopa kusema vibaya juu ya mutumishi wangu Musa? Hapo Yawe akawaka hasira juu yao, akaondoka, akaenda zake. Wingu lilipoondoka juu ya hema la mukutano, Miriamu akaonekana yuko na ukoma, mweupe kama teluji. Haruni alipogeuka na kumwangalia Miriamu, akashangaa kuona kwamba ameshikwa na ukoma. Hapo, Haruni akamwambia Musa: Ewe bwana wangu, tumetenda mambo ya kipumbafu na kufanya zambi. Lakini usituazibu! Usimufanye Miriamu akuwe kama mutu aliyezaliwa mufu, ambaye karibu nusu ya mwili wake imeozeshwa. Musa akamulilia Yawe akisema: Ninakusihi, ee Mungu, umuponye. Lakini Yawe akamwambia Musa: Kama baba yake angemutemea mate kwenye uso, basi, hangepata haya kwa siku saba? Basi, umutoe inje ya kambi akae kule muda wa siku saba, kisha unaweza kumuruhusu arudi katika kambi. Kwa hiyo, Miriamu akafukuzwa inje ya kambi kwa muda wa siku saba. Watu hawakuanza tena safari mpaka Miriamu aliporudishwa tena katika kambi. Nyuma ya hayo, watu wakafanya safari kutoka Haseroti, wakapiga kambi katika jangwa la Parani. Yawe akamwambia Musa: Tuma watu waende wapeleleze inchi ya Kanana ambayo ninawapa watu wa Israeli. Utatuma mutu mumoja kutoka katika kila kabila, na mutu huyo anapaswa kuwa kiongozi katika kabila lake. Basi, kwa agizo la Yawe, Musa akatuma watu kutoka jangwa la Parani. Watu wote waliotumwa walikuwa viongozi wa makabila mbalimbali ya watu wa Israeli. Haya ndiyo majina ya watu ambao Musa aliwatuma kwenda kupeleleza inchi ya Kanana. Musa akamupa Hosea mwana wa Nuni jina jipya, akamwita Yoshua. Alipowatuma kwenda kupeleleza inchi ya Kanana, Musa akawaambia: Muende kule ngambo Negebu, mpaka kwenye inchi ya milima, mupeleleze jinsi inchi inavyokuwa. Muchunguze vilevile kama watu wanaoishi mule ni wenye nguvu au wazaifu, wengi au wachache. Mupeleleze kama inchi hiyo ni nzuri au mbaya, na kama miji wanamoishi ni kambi au ni nyumba zilizozungukwa na kuta. Muchunguze vilevile kama inchi yenyewe ni tajiri au masikini, ina miti au haina. Mukuwe na mioyo ya ushujaa na munaporudi mulete matunda ya inchi hiyo. Ilikuwa ni wakati zabibu zinapoanza kuivya. Basi, watu hao wakaenda na kupeleleza inchi toka jangwa la Sini mpaka Rehobu, karibu na njia ya kuingilia Hamati. Wakakwenda mpaka Negebu wakapita mpaka muji wa Hebroni. Humo wakawakuta Waahimani, Wasesai na Watalmai, wazao wa Anaki. (Muji wa Hebroni ulikuwa umejengwa miaka saba mbele ya muji wa Soani unaokuwa katika inchi ya Misri). Walipofika katika Bonde la Eskoli, watu hao wakakata shada la muzabibu lililokuwa na matunda mengi nalo lilibebwa na watu wawili juu ya muti. Wakatwaa vilevile makomamanga na tini. Pahali pale pakaitwa Bonde la Eskoli, ni kusema “Bonde la Shada” kwa sababu ya shada ambalo watu hao wa Israeli walikata kutoka pahali pale. Kisha kupeleleza inchi kwa muda wa siku makumi ine, watu hao wakarudi. Wakawaendea Musa, Haruni na Waisraeli wote pamoja kule Kadesi, katika jangwa la Parani, wakatoa habari ya mambo waliyoona na kuwaonyesha matunda ya inchi. Wakamwambia Musa: Tuliifikia inchi uliyotutuma tuipeleleze; hiyo ni inchi inayotiririka maziwa na asali, na hili ni tunda lake. Lakini wenyeji wake ni wenye nguvu sana, na miji yao ni imara na mikubwa sana. Zaidi ya hayo, huko tuliona wazao wa Anaki. Waamaleki wanakaa katika eneo la Negebu; Wahiti, Wayebusi na Waamori wanakaa katika eneo la milima, na Wakanana wanakaa karibu na bahari ya Mediteranea na karibu na kingo za muto Yordani. Lakini Kalebu akanyamazisha watu mbele ya Musa, akasema: Tuende mara moja tuitwae inchi hiyo. Kwa sababu tuko na uwezo sana wa kushinda. Lakini watu walioandamana naye kupeleleza inchi wakasema: Hatutaweza kupigana na watu hao; wao wana nguvu kuliko sisi. Kwa hiyo wakaeneza mambo ya uongo kati ya watu wa Israeli juu ya inchi waliyoipeleleza, wakisema: Inchi hiyo inawaua watu wake. Vilevile watu wote tuliowaona huko ni wakubwa sana. Tuliona majitu huko, wazao wa Anaki. Sisi tulijiona kuwa kama mapanzi mbele yao, na ndivyo walivyotuona sisi. Waisraeli wote pamoja wakalalamika na kulia usiku ule. Wakamunungunikia Musa na Haruni wakisema: Afazali tungekufia Misri! Afazali tungekufia hapahapa katika jangwa! Kwa nini Yawe anatupeleka katika inchi hiyo? Tutauawa katika vita, na wake zetu na watoto wetu watakamatwa mateka! Si afazali turudi Misri? Basi wakaanza kuambiana: Tuchague kiongozi, turudi Misri. Hapo, Musa na Haruni wakaanguka uso mpaka chini mbele yao. Yoshua mwana wa Nuni, na Kalebu mwana wa Yefune, ambao walikuwa kati ya wale watu waliokwenda kupeleleza hiyo inchi, wakararua nguo zao na kuwaambia Waisraeli: Inchi tuliyokwenda kupeleleza ni nzuri sana. Ikiwa Yawe amependezwa nasi, atatupeleka huko na kutupatia inchi inayotiririka maziwa na asali. Lakini musimwasi tu Yawe, wala musiwaogope wenyeji wa inchi hiyo. Maana wao ni kama mboga tu kwetu. Kingo yao imekwisha kuondolewa kwao naye Yawe yuko pamoja nasi. Musiwaogope! Lakini wengine wote pamoja wakatishia kuwapiga mawe. Kwa rafla, utukufu wa Yawe ukatokea juu ya hema la mukutano, mbele ya watu wote wa Israeli. Kisha Yawe akamwambia Musa: Watu hawa watanizarau mpaka wakati gani? Na mpaka wakati gani wataendelea kutoniamini, hata pamoja na vitambulisho vyote nilivyotenda kati yao? Nitawapiga kwa ugonjwa mukali na kuwatupilia mbali; lakini, kutokana nawe, nitaunda taifa lingine kubwa, lenye nguvu kuliko wao. Lakini Musa akamwambia Yawe: Uliwatoa watu hawa katika inchi ya Misri kwa nguvu yako. Wamisri watakaposikia kwamba umewatendea watu wako hivyo, watawapasha wakaaji wa inchi habari hii. Maana watu hawa wamekwisha kupata habari kwamba wewe, ee Yawe, uko pamoja nasi; maana wewe, ee Yawe, unaonekana waziwazi wingu lako linaposimama juu yetu, na kwamba wewe unatutangulia muchana kwa nguzo ya wingu na usiku kwa nguzo ya moto. Sasa basi, ukiwaua watu wako wote kwa mara moja, mataifa ambayo yamekwisha kusikia sifa zako yatasema: Yawe aliwaua watu wake katika jangwa kwa sababu alishindwa kuwapeleka katika inchi aliyoahidi kuwapa. Basi, sasa ninakusihi, ee Yawe, utuonyeshe uwezo wako kwa kufanya kama ulivyotuahidi uliposema: “Mimi Yawe si mwepesi wa hasira, ni mwenye wema mwingi, na ni mwenye kusamehe uovu na makosa. Lakini kwa vyovyote vile sitakosa kuwaazibu watoto na wajukuu mpaka kizazi cha tatu na cha ine kwa zambi za wazazi wao.” Ninakusihi uwasamehe watu hawa zambi zao, kadiri ya wema wako mwingi kama vile ulivyowasamehe tangu watoke Misri mpaka sasa. Yawe akajibu: Nimewasamehe kama vile ulivyoomba. Lakini kwa kweli, kama vile ninavyoishi na kama vile dunia itakavyojaa utukufu wa Yawe, hakuna hata mumoja wao ambaye amekwisha kuuona utukufu wangu na vitambulisho vyangu nilivyofanya Misri na katika jangwa kisha akazidi kunijaribu mara hizi zote bila ya kutii sauti yangu, atakayeona inchi ile niliyoapa kuwapatia babu zao. Vilevile hata wale wanaonizarau hawataiona. Lakini kwa sababu mutumishi wangu Kalebu ni tofauti, na amenitii kwa ukamilifu, nitamufikisha kwenye inchi hiyo aliyoingia ndani yake na wazao wake watairizi. Kwa sababu Waamaleki na Wakanana wanakaa katika mabonde ya inchi hiyo, kesho mugeuke nyuma muende katika jangwa kuelekea bahari ya Shamu. Kisha Yawe akamwuliza Musa na Haruni: Kundi hili la watu waovu litaendelea kuninungunikia mpaka wakati gani? Nimechoka na haya manunguniko ya Waisraeli juu yangu! Sasa uwajibu hivi: Yawe anasema hivi: Kama vile ninavyoishi, nitawatendea ninyi yaleyale niliyosikia mukiyasema: Mutakufa na miili yenu itatupwa humuhumu katika jangwa, kwa sababu mumenungunika juu yangu, hakuna hata mumoja wenu mwenye umri wa kuanzia miaka makumi mbili na zaidi, atakayeingia katika inchi hiyo ambayo niliapa kuwapa ikuwe yenu, isipokuwa Kalebu mwana wa Yefune, na Yoshua mwana wa Nuni. Ninyi mulisema kwamba watoto wenu watakamatwa mateka, lakini mimi nitawafikisha watoto wenu katika inchi muliyoizarau, kusudi waijue na ikuwe makao yao. Lakini ninyi, mutakufia humuhumu katika jangwa. Watoto wenu watatangatanga na kutaabika humu katika jangwa kwa muda wa miaka makumi ine kwa ajili ya ukosefu wenu wa imani mpaka mutu wenu wa mwisho atakapokufia katika jangwa. Kutokana na makosa yenu, mutataabika kwa muda wa miaka makumi ine, sawa na zile siku makumi ine mulizopeleleza ile inchi, mwaka mumoja kwa kila siku moja; mutatambua kwamba mimi nimechukizwa. Mimi Yawe nimesema: Hakika nitawatendea hivyo ninyi wote muliokusanyika hapa kwa kunipinga. Wote wataishia humuhumu katika jangwa na ni humu watakamokufia. Wale watu ambao Musa aliwatuma kwenda kupeleleza ile inchi waliorudi na kusababisha watu wamunungunikie Yawe kwa kuleta habari ya uongo juu ya inchi, watu hao waliotoa habari za uongo juu ya hiyo inchi, wakakufa kwa pigo mbele ya Yawe. Lakini Yoshua mwana wa Nuni, na Kalebu mwana wa Yefune, wakabaki wazima kati ya wale watu waliokwenda kupeleleza inchi. Musa akawaambia Waisraeli wote nao wakalia kwa uchungu mwingi. Kesho yake, wakaamuka asubui mapema wakaenda sehemu za milima, wakisema: Sasa tuko tayari kabisa kwenda pahali ambapo Yawe alituahidi. Tunaitika kwamba tulitenda zambi. Lakini Musa akasema: Sasa mbona munavunja agizo la Yawe? Hivyo hamutashinda! Musiende kule kwenye milima kusudi musipigwe bure na waadui zenu, maana, Yawe hayuko pamoja nanyi. Mukiwashambulia Waamaleki na Wakanana, mutakufia katika vita kwa sababu mumeacha kumufuata Yawe. Yeye hatakuwa pamoja nanyi. Hata hivyo, wao wakakazana kwenda juu kwenye milima, ingawa Sanduku la Agano la Yawe, wala Musa hakuondoka katika kambi. Halafu Waamaleki na Wakanana, waliokuwa wakiishi katika inchi hiyo ya milima, wakashuka, wakawashambulia na kuwashinda. Wakawafukuza mpaka muji wa Horma. Yawe akamwambia Musa: Uwaambie Waisraeli kwamba mutakapofika katika inchi ninayowapa ambamo mutaishi, mukinitolea mimi Yawe sadaka kutoka katika mifugo yenu, sadaka ya kuteketezwa au sadaka ya kutimiza kiapo au kutoa sadaka ya mapenzi au sadaka ya wakati wa sikukuu zenu zilizowekwa, na kufanya harufu nzuri ya kunipendeza mimi Yawe, basi, yule anayetoa sadaka yake, atamuletea vilevile Yawe sadaka ya vyakula ya kilo moja ya unga laini uliopondwa na kuchanganywa na litre moja ya mafuta. Toa litre moja ya divai kama sadaka ya kinywaji kwa kila mwana-kondoo wa sadaka ya kuteketezwa kwa moto au sadaka ingine. Wakati wa kutoa sadaka ya kondoo dume, kilo mbili za unga uliopondwa na litre moja na nusu ya mafuta vitatolewa kama sadaka ya vyakula, pamoja na sadaka ya kinywaji ya litre moja na nusu ya divai, na kufanya harufu nzuri ya sadaka ya kumupendeza Yawe. Wakati mutakapomutolea Yawe mwana-ngombe dume kwa ajili ya sadaka ya kuteketezwa au sadaka kwa kutimiza kiapo au kwa ajili ya sadaka za amani, mutu atamutoa kama vile sadaka pamoja na sadaka ya vyakula ya unga wa kilo tatu unaokuwa muzuri na litre mbili za mafuta, pamoja na sadaka ya kinywaji ya litre mbili za divai, na kufanya harufu nzuri ya sadaka ya kumupendeza Yawe. Hivi ndivyo vitu vitakavyotolewa pamoja na kila mwana-ngombe dume, kondoo dume au mbuzi. Hesabu ya vitu hivyo itaongezwa kulingana na hesabu ya nyama watakaotolewa. Kila mwananchi Mwisraeli atafuata maagizo hayo wakati anapotoa sadaka, harufu inayomupendeza Yawe. Na kama kuna mugeni anayeishi pamoja nanyi kwa muda au siku zote, akitaka kutoa sadaka yake kwa kuiteketeza kwa moto, harufu inayomupendeza Yawe, mutu huyo atafanya kama vile munavyofanya ninyi. Katika vizazi vyote vinavyokuja, masharti yaleyale mutakayofuata ninyi ndiyo mugeni yeyote atakayeishi pamoja nanyi atakayofuata; mbele ya Yawe mutakuwa sawa. Ninyi na yeye mutakuwa chini ya sheria ileile moja na maagizo yaleyale. Yawe akamwambia Musa: Uwaambie Waisraeli kwamba wakati watakapoingia katika inchi ninayowapeleka ndani yake kila mara mutakapokula mazao ya inchi hiyo, mutatenga sehemu fulani na kunipa mimi Yawe. Mutakapopika mukate, mukate wa kwanza wa mazao ya kwanza ya ngano yenu utatolewa kama sadaka kutoka pahali pa kupepetea ngano. Mutanitolea mimi Yawe sadaka hii katika vizazi vyenu vyote vinavyokuja. Lakini kama mutakosa kufuata amri zote ambazo mimi Yawe nimewapa kwa njia ya Musa, kama siku zinazokuja watu hawatafuata yote ambayo mimi Yawe nimemwamuru Musa, basi, ikiwa kosa hilo limefanyika bila kukusudia, bila Waisraeli wote pamoja kujua, watatoa mwana-ngombe dume mumoja kuwa sadaka ya kuteketezwa kwa moto, harufu nzuri ya kumupendeza Yawe, pamoja na sadaka yake ya vyakula na ya kinywaji kufuatana na maagizo yake. Vilevile watu watatoa beberu mumoja kuwa sadaka kwa ajili ya zambi. Kuhani atafanya upatanisho kwa ajili ya Waisraeli wote pamoja, nao watasamehewa kwa sababu si kosa lililokusudiwa, na wameleta sadaka yao, sadaka ya kuteketezwa kwa Yawe kama sadaka ya zambi kwa ajili ya kosa lao. Waisraeli wote, pamoja na wageni wanaoishi nao, watasamehewa kwa sababu wote walielekewa na kosa hilo. Mutu mumoja akifanya zambi bila kujua, atatoa mbuzi dike wa mwaka mumoja kuwa sadaka kwa ajili ya zambi. Kuhani atafanya upatanisho mbele ya Yawe, kwa ajili ya huyo mutu aliyekosa bila kujua, naye atasamehewa. Mutafuata sheria moja kila mutu atakayekosa bila kukusudia, akuwe ni mwanainchi Mwisraeli au ni mugeni anayeishi pamoja nanyi. Lakini mutu yeyote atakayekosa kwa makusudi, akuwe mwanainchi au mugeni, atakuwa amemutukana Yawe, na anapaswa kutengwa mbali kati ya watu wake. Maana amekataa neno la Yawe na kuvunja moja kati ya amri zake. Mutu huyo atatengwa mbali kabisa; na lazima ya kifo chake itakuwa juu yake mwenyewe. Siku moja, wakati Waisraeli walipokuwa katika jangwa, wakamwona mutu mumoja akiokota kuni siku ya Sabato. Basi, mutu huyo akapelekwa mbele ya Musa, Haruni na Waisraeli wengine wote. Wao wakamuweka katika kifungo kwa sababu haikukuwa bado imesemwa wazi namna ya kumufanya mutu wa namna hiyo. Halafu Yawe akamwambia Musa: Mutu huyo anapaswa kuuawa; Waisraeli wote pamoja watamupiga mawe inje ya kambi. Basi, watu wakamutoa inje ya kambi, wakamupiga mawe mpaka akakufa, kama vile Yawe alivyomwamuru Musa. Kisha Yawe akamwambia Musa: Uwaambie watu wa Israeli, uwaagize wajifanyie vishada katika incha za nguo zao, na kutia nyuzi za rangi ya samawi juu ya kila kishada. Uwaambie wafanye hivyo katika vizazi vyao vyote vinavyokuja. Vishada hivyo vitakuwa ukumbusho kwenu. Kila mara mutakapoviona, mutakumbuka amri zangu zote na kuzifuata, kusudi musifuate mapenzi yenu na yale munayoona kwa macho yenu wenyewe. Vishada hivyo vitawakumbusha amri zangu zote na mutazifuata zote kwa ukamilifu, nanyi mutakuwa watakatifu wangu. Mimi ni Yawe, Mungu wenu, niliyewatoa katika inchi ya Misri kusudi nikuwe Mungu wenu. Mimi ni Yawe, Mungu wenu. Kisha Kora mwana wa Isihari mwana wa Kohati mwana wa Lawi, akatwaa watu pamoja na watu watatu wa ukoo wa Rubeni: Datani na Abiramu, wana wa Eliabu, na Oni mwana wa Peleti. Hao wote waliungwa mukono na viongozi wenye heshima mia mbili makumi tano waliochaguliwa na Waisraeli, wakamwasi Musa. Wakakusanyika mbele ya Musa na Haruni, wakawaambia: Ninyi mumepitisha kipimo! Waisraeli wote pamoja ni watakatifu; kila mumoja ni mutakatifu. Yawe yuko pamoja nasi wote. Mbona sasa ninyi munajifanya wakubwa kushinda watu wengine wa Yawe? Musa aliposikia hayo, akajitupa uso mpaka chini. Kisha akamwambia Kora na wafuasi wake: Kesho asubui, Yawe ataonyesha ni nani anayekuwa wake na ni nani anayekuwa mutakatifu, na yule atakayemuchagua, atamuwezesha kukaribia kwenye mazabahu. Basi, mufanye hivi: asubui, wewe pamoja na wafuasi wako, mutatwaa vyetezo, muweke makaa ya moto ndani na kutia ubani juu yake, kisha mutavipeleka mbele ya Yawe. Halafu tutaona ni nani aliyechaguliwa na Yawe. Ninyi Walawi mumepitisha kipimo! Musa akaendelea kumwambia Kora: Musikilize, enyi Walawi! Munaona ni jambo dogo kwenu kwamba Mungu wa Israeli amewachagua ninyi kati ya Waisraeli wote, kusudi muweze kumukaribia na kutumika katika hema la Yawe na kushugulika na kutumikia Waisraeli wote? Amewapatia heshima ya kuwa karibu naye, ninyi pamoja na Walawi wenzenu wote. Sasa munataka vilevile kazi ya ukuhani? Si Haruni tu munayemunungunikia, wewe na kundi lako, lakini kwa kweli munamwasi Yawe. Musa akatuma ujumbe kwa Datani na Abiramu wana wa Eliabu kusudi waitwe, lakini wao wakasema: Hatutakuja! Ni jambo dogo kwamba umetutoa Misri, inchi inayotiririka maziwa na asali, kusudi ukuje kutuua humu katika jangwa? Tena, unajifanya mukubwa wetu! Zaidi ya hayo, haukutuleta katika inchi inayotiririka maziwa na asali, wala kutupatia urizi wa mashamba na mashamba ya mizabibu. Unafikiri utawafanya hawa watu kuwa vipofu? Hatutakuja! Musa akakasirika sana, akamwambia Yawe: Usikubali sadaka za watu hawa. Mimi sijatwaa punda wa mutu yeyote, wala sijamuzuru mutu! Musa akamwambia Kora: Kesho usikose kuja pamoja na wafuasi wako mbele ya Yawe. Haruni vilevile atakuwa pale. Kila mumoja wenu atwae chetezo chake, na kutia ubani, kisha atakipeleka mbele ya Yawe; kwa jumla vitakuwa vyetezo mia mbili makumi tano; wewe vilevile na Haruni, kila mumoja atakuwa na chetezo chake. Basi, kila mumoja wao akatwaa chetezo chake, akatia makaa ya moto na ubani, kisha wakaenda na kusimama kwenye mulango wa hema la mukutano, pamoja na Musa na Haruni. Naye Kora akawakusanya watu wote pamoja, wakasimama mbele ya Musa na Haruni ambao walikuwa kwenye mulango wa hema la mukutano. Halafu utukufu wa Yawe ukawatokea watu wote. Hapo Yawe akamwambia Musa na Haruni: Mujitenge na watu hawa, niwaangamize sasa hivi. Lakini Musa na Haruni wakajitupa uso mpaka chini na kusema: Ee Yawe unayekuwa asili ya uzima wa wanadamu wote. Mutu mumoja akikukosea, utakasirikia watu wote pamoja? Yawe akamwambia Musa: Uwaambie watu waondoke karibu na makao ya Kora, Datani na Abiramu. Basi, Musa akaenda kwa Datani na Abiramu, akifuatwa na wazee wa Israeli. Alipofika, akawaambia watu: Tafazali muondoke kwenye hema za watu hawa waovu na musiguse kitu chao chochote, musiangamizwe pamoja nao kwa sababu ya zambi zao zote. Watu wakaondoka kwenye makao ya Kora, Datani na Abiramu. Datani na Abiramu wakatoka katika mahema yao na kusimama kwenye mulango wakiandamana na wake zao na watoto wao wote hata wale wanaonyonya. Hapo Musa akawaambia watu: Hivi ndivyo mutakavyotambua kwamba Yawe ndiye aliyenituma kufanya mambo haya yote, wala siyo kwa mapenzi yangu mwenyewe. Watu hawa wakikufa kifo cha kawaida, au wakipatwa na hasara kama watu wengine, basi mujue kwamba Yawe hakunituma. Lakini Yawe akifanya jambo ambalo halijapata kutendeka, udongo ukifunguka na kuwameza watu hawa pamoja na kila kitu chao, na kwenda kuzimu wakiwa uzima, basi mutajua kwamba watu hawa wamemuzarau Yawe. Mara tu alipomaliza kusema maneno hayo yote, udongo chini ya Datani na Abiramu ikafunuka na kuwameza watu hao, jamaa zao, pamoja na wafuasi wote wa Kora na mali zao zote. Basi, wao, pamoja na vyote vilivyokuwa vyao wakashuka kuzimu wakiwa wangali wazima. Udongo ukawafunika, wote wakatoweka. Waisraeli wote wengine waliokuwa karibu waliposikia vilio vyao wakakimbia wakisema: Tukimbie, kusudi udongo usitumeze na sisi vilevile. Kisha Yawe akashusha moto ukawateketeza wale watu mia mbili makumi tano waliokwenda kufukiza ubani. Nyuma ya hayo, Yawe akamwambia Musa: Umwambie Eleazari mwana wa kuhani Haruni atoe hivyo vyetezo kwenye moto, atupe mbali moto unaokuwa ndani, maana vyetezo hivyo ni vitakatifu. Vimekuwa vitakatifu kwa sababu watu hawa walivileta kwenye mazabahu ya Yawe. Basi, utwae vyetezo vya watu hao waliouawa kwa sababu ya zambi zao, vifuliwe kuwa vyembamba kusudi vikuwe kifuniko cha mazabahu. Hili litakuwa onyo kwa Waisraeli wote. Basi, kuhani Eleazari akatwaa vyetezo hivyo vya shaba ambavyo vililetwa mbele ya Yawe na wale watu walioteketezwa vikafuliwa kuwa kifuniko cha mazabahu. Hili lilikuwa onyo kwa Waisraeli kwamba mutu yeyote ambaye si kuhani, maana yake asiyekuwa wa ukoo wa Haruni asiende kwenye mazabahu kwa kumufukizia Yawe ubani. Kama sivyo ataangamizwa kama Kora na wafuasi wake. Haya yote yalitendeka kama vile Yawe alivyomwambia Eleazari kwa njia ya Musa. Kesho yake, Waisraeli wote pamoja wakamunungunikia Musa na Haruni wakisema: Mumewaua watu wa Yawe. Walipokusanyika mbele ya Musa na Haruni kwa kutoa malalamiko yao, wakageuka kuelekea hema la mukutano, wakaona kwamba wingu limeifunika hema na utukufu wa Yawe ulikuwa umetokea pale. Musa na Haruni wakakwenda, wakasimama mbele ya hema la mukutano, na Yawe akamwambia Musa: Ujitenge na watu hawa, niwaangamize mara moja! Lakini wao wakajitupa uso mpaka chini. Musa akamwambia Haruni: Twaa chetezo chako, utie moto ndani yake na kukiweka kando ya mazabahu, kisha utie ubani halafu uende nacho haraka kwa watu na kuwafanyia upatanisho. Fanya haraka! Kasirani ya Yawe imekwisha kuwafikia na pigo limeanza kuwashambulia. Basi, Haruni akafanya kama vile alivyoambiwa na Musa. Akatwaa chetezo chake na kukimbia mpaka katikati ya watu waliokuwa wamekusanyika pamoja. Alipoona kwamba pigo limekwisha kuanza, akatia ubani katika chetezo na kuwafanyia watu upatanisho. Alipofanya hivyo, pigo hilo likakoma, naye akabaki katikati ya waliokufa na waliokuwa wazima. Hesabu ya watu waliokufa kwa pigo ilikuwa elfu kumi na ine mia saba, bila kuhesabu wale waliokufa kutokana na uasi wa Kora. Pigo lilipokoma, Haruni akarudi kwa Musa kwenye mulango wa hema la mukutano. Kisha Yawe akamwambia Musa: Uwaambie Waisraeli wakuletee fimbo kumi na mbili, kila kiongozi wa kabila fimbo moja. Uandike jina la kila mumoja wao kwenye fimbo yake, na jina la Haruni uliandike juu ya fimbo inayosimamia kabila la Lawi. Kutakuwa fimbo moja kwa kila kiongozi wa kabila. Upeleke fimbo hizo katika hema la mukutano na kuziweka mbele ya Sanduku la Agano, pahali ambapo mimi ninakutana nawe. Fimbo ya mutu nitakayemuchagua itachipuka. Kwa njia hii nitakomesha manunguniko ya Waisraeli juu yenu. Musa akaongea na watu wa Israeli. Viongozi wao wote wakamupa kila mumoja fimbo yake kulingana na kabila lake kwa jumla zikakuwa fimbo kumi na mbili. Fimbo ya Haruni ikawekwa pamoja na fimbo hizo. Musa akaziweka fimbo hizo zote mbele ya Yawe katika hema la mukutano. Kesho yake asubui, Musa akakwenda katika hema la mukutano. Mule, akakuta fimbo ya Haruni wa kabila la Lawi, imechipuka na kutoa vifundo vilivyochanua maua na kuzaa matunda mabichi ya lozi. Kisha Musa akatoa fimbo zote hapo mbele ya Yawe, akawaonyesha Waisraeli wote, na kila kiongozi akatwaa fimbo yake. Yawe akamwambia Musa: Urudishe fimbo ya Haruni mbele ya Sanduku la Agano. Hiyo itatunzwa pahali pale, na ni onyo kwa waasi hao kwamba wasipoacha kuninungunikia, watakufa. Musa akafanya kama vile alivyoamriwa na Yawe. Waisraeli wakamwambia Musa: Angalia sasa! Tunaangamia! Tumekwisha! Wote tumekwisha. Kila mutu atakayekaribia hema la Yawe atakufa. Tutaangamia sisi wote? Basi, Yawe akamwambia Haruni: Wewe na wana wako na ukoo wako mutabeba lazima ya kazi za hema takatifu; vilevile na makosa yanayoambatana na ukuhani wako wewe mwenyewe na wana wako. Wewe, wana wako na wazao wako wote mutatumika kama vile makuhani; wandugu zako wengine wa kabila lako watafanya kazi pamoja nawe mbele ya hema la kuchunga vibao vya agano. Wao watafanya kazi utakazowapa na kutimiza mapaswa yao juu ya hema. Lakini hawana ruhusa ya kugusa vyombo vya hema, wala kukaribia mazabahu, kusudi wasikufe, nawe vilevile usikufe. Wao watajiunga nawe katika kazi na kutimiza mapaswa yao kwa ukamilifu juu ya kazi zote za hema, wala kusikuwe mutu mwingine atakayekukaribia mule. Ninyi mutafanya kazi za Pahali Patakatifu na mazabahu, kusudi kasirani yangu isiwatokee tena Waisraeli. Ni mimi niliyewachagua wandugu zenu Walawi kati ya Waisraeli kama vile toleo kwenu. Wao wametengwa kwa ajili yangu mimi Yawe, kusudi wafanye kazi katika hema la mukutano. Lakini wewe peke yako na wana wako mutafanya kazi zote za kikuhani kwa ajili ya mazabahu na vyote vinavyokuwa ndani ya pazia. Hayo ni mapaswa yenu, kwa sababu ninawapa zawadi ya ukuhani. Mutu yeyote asiyestahili atakayekaribia vyombo vya hema, atauawa. Yawe akamwambia Haruni: Ninakupatia matoleo Waisraeli waliyonipa, vitu vyote vitakatifu walivyonipa: vitu vyote vilivyotakaswa na Waisraeli. Ninakupa vitu vyote wewe na wazao wako kuwa fungu lenu, na hiyo ni haki yenu milele. Kati ya vitu vitakatifu kabisa ambavyo haviteketezwi kwa moto, hivi vitakuwa vyenu: sadaka za vyakula, sadaka kwa ajili ya zambi na sadaka za kosa. Kila kitu watu watakachonitolea kama vile sadaka takatifu kitakuwa chako na wana wako. Mutavikula vitu hivyo kama vitu vitakatifu kabisa, na ni wanaume tu ndio watakaovikula; vitu hivyo ni vitakatifu kwenu. Vilevile, vitu vingine vyote Waisraeli watakavyonitolea kama vile sadaka za kutikiswa, vitakuwa vyako. Ninakupa wewe, wana wako na wabinti zako kuwa haki yenu milele. Mutu yeyote katika jamaa yako asiyekuwa muchafu anaweza kula vitu hivyo. Ninakupa vitu vyote vizuri vinavyotokana na malimbuko ambayo Waisraeli wananitolea: mafuta safi, divai na ngano. Mazao yote ya kwanza ya matunda mabichi ya mashamba yao ambayo wataniletea mimi, yatakuwa yako. Kila mutu asiyekuwa muchafu katika jamaa yako anaweza kula. Kila kitu kilichotakaswa katika inchi ya Israeli kitakuwa chenu. Kila muzaliwa wa kwanza ambaye Waisraeli watanitolea, akiwa muzaliwa wa kwanza wa wanadamu, au wa nyama, atakuwa wako. Lakini unaweza kuwakomboa wazaliwa wa kwanza wote wa wanadamu, na kila muzaliwa wa kwanza wa nyama anayekuwa muchafu. Wazaliwa hao wa kwanza watakombolewa wakiwa wenye umri wa mwezi mumoja kwa kulipiwa feza shekeli tano, kulingana na vipimo vya hema takatifu. Lakini wazaliwa wa kwanza wa ngombe, kondoo au mbuzi wasikombolewe; hao ni watakatifu. Damu yao utainyunyizia mazabahu na mafuta yao utayateketeza kuwa sadaka ya kuteketezwa ambayo ni harufu nzuri inayonipendeza mimi Yawe. Nyama yao unaweza kuikula, kama vile kilali na muguu wa nyuma wa kuume vinavyotolewa kama vile sadaka ya kutikiswa. Ninakupa wewe, wana wako na wabinti zako, vitu vyote ambavyo watu wa Israeli wananitolea; hivyo ni haki yenu siku zote. Hili ni agano la milele mbele yangu ambalo ni kwa ajili yako na wazao wako. Yawe akamwambia Haruni: Wewe hautakuwa na urizi wowote katika inchi yao, wala kuwa na fungu lako kati yao; mimi ni fungu lako na urizi wako kati ya Waisraeli. Kuelekea Walawi, hao nimewapa sehemu ya kumi ya kila kitu Waisraeli wanachonitolea kuwa urizi wao. Haya yatakuwa malipo yao kwa kazi wanayotoa katika kulitunza hema la mukutano. Na tangu sasa, watu wengine wa Israeli wasikaribie hema la mukutano kusudi wasitende zambi na kujiletea kifo. Lakini Walawi peke yao ndio watakaotumika katika hema la mukutano; na kuwa na mapaswa kwa ukamilifu juu yake. Hili ni sharti la kufuata siku zote katika vizazi vyenu vyote. Walawi hawatakuwa na mali ya kurizi katika inchi ya Israeli, kwa sababu sehemu ya kumi Waisraeli wanayonitolea nimewapa kuwa urizi wao. Ndiyo maana nimesema kwamba wao hawatakuwa na urizi kati ya Waisraeli. Kisha, Yawe akamwambia Musa: Tena utawaambia Walawi maagizo haya: Wakati mutakapopokea sehemu ya kumi ambayo Yawe amewapa kutoka kwa Waisraeli ikuwe urizi wenu, mutanitolea mimi Yawe sehemu moja ya kumi ya vitu hivyo. Sadaka hii yenu itakubaliwa kuwa kama malimbuko ya ngano au kama zabibu mulimaji anazonitolea. Basi, ndivyo, mutakavyonitolea mimi Yawe sadaka ya sehemu ya kumi mutakazopokea kutoka kwa Waisraeli. Sehemu hiyo ya kumi mutakayonitolea mimi Yawe mutamupa kuhani Haruni. Kutokana na matoleo yote mutakayopokea, mutamutolea Yawe sehemu inayokuwa bora kuliko zote na takatifu. Kwa hiyo utawaambia: Mukisha kunitolea sehemu bora kuliko zote, sehemu itakayobakia itakuwa yenu, kama vile inavyokuwa kwa mulimaji anatwaa kinachobakia kisha kutoa sadaka zake za mazao ya kwanza ya ngano na zabibu. Nanyi mutakula kilichotolewa mukiwa pahali popote pamoja na jamaa zenu maana ni mushahara wenu kwa sababu ya kazi yenu katika hema la mukutano. Hamutakuwa na kosa lolote mukikula vitu hivyo, ikiwa kama mumemutolea Yawe sehemu bora kuliko zote, nanyi hamutachafua vitu vitakatifu vya Waisraeli na kufa. Yawe akawaambia Musa na Haruni: Haya ni masharti ya sheria ambayo mimi Yawe ninatoa. Uwaambie Waisraeli wawaletee ngombe dike mwekundu mukamilifu asiyekuwa na kilema chochote, na ambaye hajapata kufungwa nira. Ninyi mutamupa kuhani Eleazari ngombe huyo. Atatolewa inje ya kambi na kuchinjwa mbele ya kuhani huyo. Kisha kuhani Eleazari atatwaa sehemu ya damu na kuinyunyiza kwa kidole mara saba, kuelekea upande wa mbele wa hema la mukutano. Ngombe huyo muzima atateketezwa kwa moto mbele ya kuhani. Kila kitu chake kitateketezwa; ngozi, nyama, damu na mavi yake. Halafu kuhani atatwaa muti wa mwerezi, hisopo na sufu nyekundu na kuvitia katika moto huo. Nyuma ya hayo, kuhani atafua nguo zake na kuoga mwili kwa maji, halafu anaweza kuingia katika kambi; atakuwa muchafu mpaka magaribi. Mutu atakayemuteketeza ngombe huyo vilevile atafua nguo zake na kuoga mwili, lakini naye vilevile atakuwa muchafu mpaka magaribi. Mutu anayekuwa safi atazoa majivu ya ngombe huyo na kuyapeleka pahali safi inje ya kambi. Yatalindwa na kutumiwa na jamii nzima ya Israeli kwa kutengeneza maji ya utakaso kwa kuondoa zambi. Mutu atakayezoa majivu ya ngombe huyo anapaswa kufua nguo zake, lakini atakuwa muchafu mpaka magaribi. Sharti hili ni la kufuata siku zote kwa Waisraeli na watu wengine watakaoishi pamoja nao. Mutu akigusa maiti ya mutu yeyote, atakuwa muchafu kwa siku saba. Siku ya tatu na ya saba mutu huyo atajitakasa kwa yale maji ya utakaso, naye atakuwa safi. Lakini akiacha kujitakasa katika siku ya tatu na ya saba, mutu huyo atabaki muchafu. Anayegusa maiti, ni kusema mwili wa mutu aliyekufa, asipojitakasa, anachafua hema la Yawe, naye atatengwa na watu wa Israeli. Mutu huyo atabaki muchafu kwa sababu hakunyunyiziwa yale maji ya utakaso. Na hii ndiyo sheria ya kufuatwa kama mutu akikufia ndani ya hema: Kila mutu atakayeingia ndani ya hema hilo, au aliyekuwa ndani ya hema hilo, atakuwa muchafu kwa siku saba. Kila chombo kinachokuwa wazi ambacho hakina kifuniko juu yake kitakuwa kichafu. Mutu yeyote akigusa mwili wa mutu aliyeuawa au aliyekufa kifo cha kawaida inje ya nyumba, au akigusa mufupa wa mutu au kaburi, atakuwa muchafu kwa siku saba. Kwa ajili ya wale waliojichafua, watatwaa majivu ya sadaka ya zambi iliyoteketezwa, majivu hayo yatachanganywa na maji ya muto. Mutu anayekuwa safi atatwaa hisopo, halafu ataichovya katika maji hayo, kisha atainyunyizia hema, vyombo vyote vinavyokuwa ndani ya hema na watu wanaokuwa ndani. Atamunyunyizia vilevile mutu aliyegusa mufupa wa mutu, au mwili wa mutu aliyeuawa au aliyekufa kifo cha kawaida, au aliyegusa kaburi. Katika siku ya tatu na ya saba, mutu anayekuwa safi atamunyunyizia mutu anayekuwa muchafu maji hayo; hivyo katika siku ya saba, atamutakasa mutu huyo anayekuwa muchafu, naye atafua nguo zake na kuoga, na magaribi atakuwa safi. Lakini mutu muchafu asipojitakasa, mutu huyo atatengwa mbali na jamii, kwa sababu anachafua hema la Yawe. Kwa vile hakunyunyiziwa maji ya utakaso, yuko muchafu. Hili ni sharti la kufuata siku zote. Mutu atakayenyunyiza maji ya utakaso atafua nguo zake; naye atakayegusa maji hayo atakuwa muchafu mpaka magaribi. Chochote mutu muchafu atakachogusa kitakuwa kichafu, na yeyote atakayekigusa kitu hicho atakuwa muchafu mpaka magaribi. Waisraeli wote wakafika katika jangwa la Sinai katika mwezi wa kwanza, wakapiga kambi yao huko Kadesi. Wakiwa huko, Miriamu akakufa na kuzikwa. Pahali pale walipopiga kambi hapakukuwa maji. Kwa hiyo watu wote pamoja wakakusanyika mbele ya Musa na Haruni. Wakagombanisha Musa wakisema: Afazali tungekufa pamoja na wandugu zetu mbele ya hema la Yawe! Kwa nini mulituleta sisi watu wa Yawe huku katika jangwa? Mulituleta kusudi tukufe pamoja na mifugo yetu? Kwa nini mulitutoa Misri na kutuleta pahali hapa pabaya hivi? Hapa si pahali pa ngano, tini, zabibu wala makomamanga. Hata maji ya kunywa hakuna! Hapo, Musa na Haruni wakaondoka kwenye mukutano wa watu, wakaenda kusimama kwenye mulango wa hema la mukutano, wakainama uso mpaka chini. Basi, utukufu wa Yawe ukawatokea, naye Yawe akamwambia Musa: Twaa ile fimbo yako, kisha wewe na ndugu yako Haruni mukusanye watu wote pamoja. Halafu, mbele ya macho yao, uambie jiwe linalokuwa mbele ya macho yao litoe maji yake. Utawatoshea maji ndani ya jiwe watu wote na mifugo yao waweze kunywa. Musa akaenda kuitwaa ile fimbo mbele ya Yawe kama vile alivyoamriwa. Kisha Musa na Haruni wakawakusanya watu wote pamoja mbele ya jiwe, naye Musa akawaambia: Musikilize sasa, enyi waasi; tuwatokezee maji kutoka katika jiwe hili? Kisha Musa akainua mukono wake, akapiga lile jiwe mara mbili kwa fimbo yake. Maji yakabubujika kwa wingi, watu wakakunywa pamoja na mifugo yao. Lakini Yawe akamwambia Musa na Haruni: Kwa sababu ninyi hamukuniamini mimi, wala kuniheshimu mbele ya macho ya Waisraeli, basi kwa sababu hiyo hamutaingiza watu hawa katika ile inchi niliyowapa. Hayo ni maji ya Meriba, ni kusema ya “Magombano”, pahali ambapo Waisraeli walimugombanisha Yawe, naye akajionyesha kwa utakatifu kati yao. Musa akatuma wajumbe kutoka Kadesi kwa mufalme wa Edomu akamwambia: Ndugu yako Israeli anasema hivi: Wewe unajua taabu zote tulizozipata. Jinsi babu zetu walivyokwenda Misri, ambako tuliishi kwa muda murefu na jinsi Wamisri walivyowatesa babu zetu, wakatutesa na sisi vilevile. Tukamulilia Yawe, naye akasikia kilio chetu, akatuletea malaika aliyetuondoa Misri. Sasa tuko hapa Kadesi, muji unaopakana na inchi yako. Tafazali uturuhusu tupite katika inchi yako. Hatutakanyaga mashamba yenu, wala yale ya mizabibu; wala hatutakunywa maji ya visima vyenu. Tutafuata barabara kubwa ya mufalme na kwenda moja kwa moja bila kugeuka kuume au kushoto, mpaka tutakapotoka katika inchi yako. Lakini mufalme wa Edomu akamujibu: Hapana! Hautapita katika inchi yangu, kama ukipita nitatoka na kukushambulia kwa upanga. Waisraeli wakamwambia: Sisi tutafuata njia kubwa; kama sisi na mifugo yetu tukikunywa maji yenu, tutalipa. Tunachoomba tafazali uturuhusu tu, tupite kwa miguu wala hatutaki neno lolote lingine. Lakini mufalme wa Edomu akajibu: Hatutawaruhusu. Mara moja, Waedomu wenye nguvu wakatoka kupigana nao. Basi, Waedomu wakakataa kuwapa Waisraeli ruhusa kwa kupita katika mipaka yao. Waisraeli wakageuka na kushika njia ingine. Waisraeli wote wakasafiri kutoka Kadesi, wakafika kwenye mulima Hori. Basi, Yawe akamwambia Musa na Haruni huko kwenye mulima Hori, kwenye mpaka wa inchi ya Edomu: Haruni atakufa; hataingia katika inchi ambayo nimewapa Waisraeli kwa sababu ninyi wawili muliasi amri yangu kule Meriba. Umutwae Haruni na mwana wake Eleazari, uwalete juu ya mulima Hori. Kisha, umuvue Haruni nguo yake, umuvalishe mwana wake Eleazari. Haruni atakufa akiwa huko kwenye mulima. Musa akafanya kama vile alivyoamriwa na Yawe. Wote watatu wakapanda juu ya mulima mbele ya watu wote wengine. Kisha Musa akamuvua Haruni nguo zake, akamuvalisha mwana wake, Eleazari. Naye Haruni akakufa palepale kwenye mulima. Kisha Musa na Eleazari wakateremuka chini. Waisraeli walipoona kwamba Haruni amekufa, wakafanya kilio cha siku makumi tatu. Mufalme mumoja Mukanana wa Aradi aliyeishi kule Negebu alipopata habari kwamba Waisraeli walikuwa wanakuja kwa njia ya Atarimu, akakwenda kuwashambulia na kuwateka wamoja kati yao. Hapo, Waisraeli wakamwekea Yawe kiapo wakisema: Kama ukiwatia watu hawa katika mikono yetu, basi tutaangamiza kabisa miji yao. Yawe akasikia ombi lao, akawapa ushindi juu ya Wakanana. Waisraeli wakaangamiza kabisa Wakanana pamoja na miji yao. Kwa hiyo pahali pale pakaitwa Horma, ni kusema “Maangamizi”. Waisraeli wakafunga safari kutoka mulima Hori, wakapitia njia inayoelekea bahari Nyekundu kusudi wazunguke inchi ya Edomu. Lakini katika njia watu wakavunjika moyo. Basi, wakaanza kumunungunikia Mungu na Musa, wakisema: Kwa nini mumetutoa Misri tukuje tukufie humu katika jangwa? Humu hamuna chakula wala maji; nasi tumechokeshwa na chakula hiki cha bure. Hapo Yawe akatuma nyoka wenye sumu kati ya watu, wakawauma hata Waisraeli wengi wakakufa. Basi, watu wakamwendea Musa, wakamwambia: Tumetenda zambi kwa kumunungunikia Yawe na wewe vilevile. Umwombe Yawe atuondolee nyoka hawa. Kwa hiyo, Musa akawaombea watu. Halafu Yawe akamwambia Musa: Tengeneza nyoka wa shaba, umutundike juu ya muti. Mutu yeyote atakayeumwa na nyoka, akiangalia kwenye nyoka huyo wa shaba, atapona. Basi, Musa akatengeneza nyoka wa shaba, akamutundika juu ya muti. Kila mutu aliyeumwa na nyoka alipomuangalia nyoka huyo wa shaba, alipona. Waisraeli wakaendelea na safari yao, wakapiga kambi kule Oboti. Kutoka kule wakasafiri mpaka Iye-Abarimu, katika jangwa upande wa mashariki wa Moabu. Kutoka kule wakasafiri wakapiga kambi yao katika bonde la Zeredi. Kutoka huko wakasafiri, wakapiga kambi upande wa kaskazini wa muto Arnoni, ambao unatiririka kutoka katika inchi ya Waamori na kupitia katika jangwa. Muto Arnoni ulikuwa mupaka kati ya Wamoabu na Waamori. Kwa sababu hiyo, imeandikwa katika kitabu cha vita za Yawe: “Muji wa Wahebu katika inchi ya Sufa, na mabonde ya Arnoni, na muteremuko wa mabonde unaofika mpaka muji wa Ari, na kuelekea kwenye mupaka wa Moabu.” Kutoka huko Waisraeli wakasafiri mpaka Beri; ni kusema kisima ambapo Yawe alimwambia Musa: Uwakusanye watu pamoja, nami nitawapa maji. Hapo Waisraeli wakaimba wimbo huu: Bubujika maji, ee kisima! Muimbe! Kisima kilichochimbwa na wakubwa kilichochimbwa sana na wenye cheo, kwa fimbo zao za utukufu na bakora. Kutoka katika jangwa wakasafiri mpaka Matana, kutoka Matana mpaka Nahalieli, kutoka Nahalieli mpaka Bamoti, na kutoka Bamoti mpaka kwenye bonde linaloingia katika inchi ya Moabu, kwenye kilele cha mulima Pisiga, kinachoelekea chini katika jangwa. Waisraeli wakamupelekea mufalme Sihoni wa Waamori, ujumbe huu: Uturuhusu tupite katika inchi yako; hatutakwenda pembeni na kuingia katika mashamba au katika mashamba ya mizabibu, wala hatutakunywa maji ya visima vyenu; tutapita moja kwa moja katika barabara kubwa ya mufalme mpaka tutakapoondoka katika inchi yako. Lakini Sihoni hakuwaruhusu Waisraeli wapite katika inchi yake. Akawakusanya watu wake, akaenda Yahasa katika jangwa kwa kuwashambulia Waisraeli. Lakini Waisraeli wakamwua kwa makali ya upanga, wakatwaa inchi yake, tangu muto Arnoni mpaka muto Yaboki, mpaka inchi ya Waamoni; nao mupaka wa inchi ya Amoni ulikuwa unalindwa sana. Waisraeli wakaiteka miji hii yote nao wakaishi katika miji ya Waamori katika Hesiboni na vijiji vyake. Hesiboni ulikuwa muji wa Sihoni mufalme wa Waamori, ambaye mbele alikuwa amepigana na mufalme wa Moabu na kuteka inchi yake yote mpaka muto Arnoni. Ndiyo maana washairi wetu wanaimba: Mukuje Hesiboni na kujenga. Muji wa Sihoni ujengwe na kuimarishwa. Maana moto ulitoka Hesiboni, miali ya moto ilitoka katika muji kwa Sihoni, ukauteketeza muji wa Ari wa Moabu, ukaiangamiza milima ya muto Arnoni. Ole wenu watu wa Moabu! Mumeangamizwa, enyi watu wa mungu Kemosi! Umewafanya watoto wenu wanaume kuwa wakimbizi, wabinti zako umewaacha watwaliwe mateka mpaka kwa Sihoni, mufalme wa Amori. Lakini sasa wazao wao wameangamizwa, kutoka Hesiboni mpaka Diboni, kutoka Nasimu mpaka Nofa, karibu na Medeba. Basi, Waisraeli wakakaa katika inchi ya Waamori. Kisha Musa akatuma watu wapeleleze muji wa Yazeri; wakauteka pamoja na vijiji vyake, wakawafukuza Waamori waliokaa humo. Waisraeli wakageuka wakafuata njia inayoenda Basani. Mufalme Ogi wa Basani akatoka na jeshi lake kwa kuwashambulia huko Edirei. Lakini Yawe akamwambia Musa: Usimwogope, maana nimemutia katika mikono yako pamoja na watu wake wote na inchi yake yote. Utamutendea kama ulivyomutendea Sihoni, mufalme wa Waamori, aliyekuwa anakaa Hesiboni. Basi, Waisraeli wakamwua Ogi, wana wake na watu wake wote, bila kumwacha hata mutu mumoja, kisha wakatwaa inchi yake. Waisraeli wakaanza safari tena, wakaenda kupiga kambi yao katika bonde za Moabu, upande wa mashariki wa muto Yordani, kuelekea muji wa Yeriko. Mufalme Balaki mwana wa Sipori, alijua mambo yote Waisraeli waliyowatendea Waamori. Yeye pamoja na Wamoabu wakashikwa na hofu kubwa juu ya Waisraeli. Waliwaogopa hasa kwa sababu ya wingi wao. Basi Wamoabu wakawaambia viongozi wa Midiani: Makundi haya ya watu sasa hivi yataharibu kila kitu kandokando yetu kama vile ngombe dume anavyokula majani katika shamba. Kwa hiyo, Balaki mwana wa Sipori aliyekuwa mufalme wa Moabu wakati ule, akapeleka ujumbe kwa Balamu mwana wa Beori, huko Petori, karibu na muto Furati katika inchi ya Amawi. Akamwambia Balamu hivi: Kuna taifa ambalo limetoka Misri, nalo limeenea kila pahali katika inchi, tena linatishia kutwaa inchi yangu. Kuja sasa uwalaani watu hawa kwa ajili yangu maana wana nguvu kuliko mimi. Labda nitaweza kuwashinda na kuwafukuza wasiingie katika inchi yangu, kwa maana unajua kwamba wewe ukimubariki mutu anabarikiwa, ukimulaani mutu analaaniwa. Basi, wazee wa Moabu na Midiani wakapeleka zawadi za uaguzi, wakaondoka kwenda kwa Balamu. Walifika, wakamupa Balamu ujumbe wa Balaki. Balamu akawaambia: Mulale huku usiku huu, nami nitawajulisha vile Yawe atakayoniambia. Basi, wazee hao wa Moabu wakakaa na Balamu. Kisha Mungu alimufikia Balamu, akamwuliza: Ni nani hawa wanaokaa nawe? Balamu akamujibu Mungu: Balaki mwana wa Sipori amenitumia ujumbe kwamba kuna watu wa taifa fulani waliotoka Misri, nao wameenea kila pahali katika inchi. Ameniomba niende kuwalaani watu hao kusudi pengine ataweza kupigana nao na kuwafukuza. Mungu akamwambia Balamu: Usiende pamoja na watu hawa, wala usiwalaani watu hao maana wamebarikiwa. Basi, asubui yake Balamu akaamuka, akawaambia wazee wa Balaki: Murudie katika inchi yenu, kwa maana Yawe hapendi kuniruhusu kwenda pamoja nanyi. Kwa hiyo wazee wa Moabu wakaondoka, wakarudi kwa Balaki, wakamwambia: Balamu amekataa kuja pamoja nasi. Kisha, Balaki akatuma wakubwa wengine, wengi zaidi na wa vyeo vya juu kuliko wale wa kwanza. Hao wakafika kwa Balamu, wakamwambia: Balaki mwana wa Sipori anasema hivi: Usikubali kuzuiwa na chochote hata uache kuja kwangu. Nitakupatia heshima kubwa, na chochote utakachoniomba nitakutimizia. Kuja uwalaani watu hawa. Lakini Balamu akawajibu watumishi wa Balaki: Hata kama Balaki atanipa nyumba yake imejaa feza na zahabu, mimi sitaweza kuvunja amri ya Yawe, Mungu wangu, juu ya jambo lolote, dogo au kubwa. Lakini tafazali mulale hapa usiku huu kama wale wenzenu, nami nipate kujua kile Yawe atakachoniambia tena. Basi, Mungu akamufikia Balamu usiku ule, akamwambia: Kama watu hawa wamekuja kukuita, kwenda pamoja nao, lakini fanya tu kile nitakachokuambia. Balamu akaamuka asubui, akatandika punda wake, akaenda pamoja na hao wakubwa. Hasira ya Mungu ikawaka kwa sababu Balamu alikuwa anakwenda; hivyo malaika wa Yawe akakutana naye katika njia. Wakati huo Balamu alikuwa amepanda juu ya punda wake naye alisindikizwa na watumishi wake wawili. Basi, punda akamwona malaika huyo wa Yawe amesimama katika njia, akishika upanga uliochomolewa. Kwa hiyo akaacha njia, akaenda pembeni. Balamu akamupiga huyo punda, akamurudisha katika njia. Kisha malaika huyo wa Yawe akatangulia mbele, akasimama pahali hiyo njia ilikuwa nyembamba, kati ya mashamba ya mizabibu na kuta pande zote mbili. Punda alipomwona malaika huyo wa Yawe, akajibanisha kwenye ukuta na kubana muguu wa Balamu hapo. Kwa hiyo Balamu akamupiga tena huyo punda. Kisha malaika akatangulia tena, akasimama pahali pembamba pasipo na nafasi ya kupita kuume wala kushoto. Punda alipomwona huyo malaika wa Yawe, akalala chini. Balamu akawaka hasira, akamupiga kwa fimbo yake. Hapo Yawe akafungua kinywa cha huyo punda, akamwambia Balamu: Nimekutendea nini hata ukanipiga mara hizi tatu? Balamu akamwambia punda: Wewe umenichekelea! Kama ningekuwa na upanga ningalikuua sasa hivi! Punda akamwambia Balamu: Mimi si yuleyule punda wako aliyekubeba maisha yako yote mpaka siku hii ya leo? Nimekwisha kukutendea namna hii? Balamu akajibu: Hapana. Hapo, Yawe akafungua macho ya Balamu, naye akamwona malaika wa Yawe amesimama katika njia, akishika upanga uliochomolewa toka kifuko chake. Balamu akajitupa uso mpaka chini. Malaika wa Yawe akamwambia Balamu: Mbona umemupiga punda wako mara tatu? Nimekuja kukuzuia, kwa sababu njia yako ni mbaya. Punda wako ameniona akaniepuka mara tatu. Kama asingaligeuka mbali nami hakika ningalikuua wewe na kumwacha muzima punda huyu. Balamu akamwambia malaika wa Yawe: Nimetenda zambi maana sikujua kwamba umesimama katika njia kwa kunizuia. Sasa, kama haikupendezi niendelee na safari hii, basi nitarudi kwangu. Lakini malaika wa Yawe akamwambia Balamu: Kwenda na watu hawa, lakini utasema tu kile nitakachokuambia. Basi, Balamu akaendelea na safari pamoja na viongozi wa Balaki. Balaki alipopata habari kwamba Balamu anakuja, akatoka kwenda kumupokea katika muji wa Ari, muji uliokuwa kwenye ukingo wa muto Arnoni kwenye mupaka wa Moabu. Balaki akamwambia Balamu: Kwa nini haukukuja kwangu mara moja nilipokuita? Ulifikiri sitaweza kukupatia heshima ya kutosha? Balamu akamujibu Balaki: Sasa nimekuja! Lakini, nina mamlaka ya kusema neno lolote? Jambo Mungu atakaloniambia ndilo ninalopaswa kusema. Basi, Balamu akaenda pamoja na Balaki. Wakafika katika muji Kiriati-husoti. Huko Balaki akatoa sadaka ya ngombe na kondoo, akawagawanyia Balamu na wakubwa waliokuwa pamoja naye nyama. Kesho yake, Balaki akamutwaa Balamu, akapanda naye mpaka Bamoti-Bali; kutoka huko, Balamu aliweza kuwaona wamoja kati ya Waisraeli. Balamu akamwambia Balaki: Unijengee mazabahu saba hapa kisha uniletee ngombe dume saba na kondoo dume saba. Balaki akafanya kama vile Balamu alivyosema. Basi, wakatolea juu ya kila mazabahu ngombe dume mumoja na kondoo dume mumoja. Halafu Balamu akamwambia Balaki: Baki hapa karibu na sadaka yako ya kuteketezwa kwa moto, nami niende. Labda Yawe atakutana nami. Chochote atakachonionyesha nitakuja kukuambia. Basi, Balamu akaenda peke yake juu ya kilele cha mulima. Mungu akakutana naye. Balamu akamwambia: Nimetayarisha mazabahu saba na kutoa ngombe dume mumoja na kondoo dume mumoja juu ya kila mazabahu. Yawe akamupa Balamu maneno atakayosema na kumwambia arudi kwa Balaki. Balamu akarudi, akamukuta Balaki akisimama palepale karibu na sadaka yake ya kuteketezwa kwa moto, pamoja na wakubwa wote wa Moabu. Balamu akamutolea Balaki mashairi yake, akasema: Balaki amenileta hapa kutoka Aramu, hakika, mufalme wa Moabu amenileta kutoka milima ya mashariki: Kuja uwalaani watu wa Yakobo kwa ajili yangu, hakika, kuja uwakaripie Waisraeli! Nitamulaani namna gani mutu ambaye Mungu hakumulaani? Nitawakaripia watu ambao Yawe hakuwakaripia? Kutoka vilele vya mawe makubwa ninawaona, kutoka juu ya milima nawachungulia, hilo taifa linalokaa peke yake, lisilojiona kuwa sawa na mataifa mengine. Nani anayeweza kuhesabu wingi wa watu wa Yakobo, au kuhesabu makundi ya Waisraeli? Nikufe kifo cha haki, mwisho wangu ukuwe kama wao. Kwa hiyo, Balaki akamwambia Balamu: Umenifanyia nini? Nimekuleta hapa uwalaani waadui zangu, lakini pahali pake umewabariki! Balamu akamwambia Balaki: Hainipasi tu kusema maneno Yawe aliyoweka ndani ya kinywa changu? Kisha, Balaki akamwambia Balamu: Tuende pahali pengine ambapo utaweza kuwaona; hata hivyo utaona tu sehemu yao, hautaweza kuwaona wote. Kisha uwalaani kutoka huko kwa ajili yangu. Basi, Balaki akamutwaa Balamu kwenye shamba la Sofimu, juu ya kilele cha mulima Pisiga. Hapo akajenga mazabahu saba na kutoa juu ya kila mazabahu ngombe dume mumoja na kondoo dume mumoja. Balamu akamwambia Balaki: Baki hapa karibu na sadaka yako ya kuteketezwa kwa moto, nami niende kule ngambo kukutana na Yawe. Yawe akakutana na Balamu, akamupa maneno atakayosema, na kumwambia arudi kwa Balaki. Basi, Balamu akarudi, akamukuta Balaki amesimama karibu na sadaka ya kuteketezwa pamoja na wakubwa wote wa Moabu. Balaki akamwuliza: Yawe amekuambia nini? Halafu, Balamu akamutolea Balaki mashairi yake: Simama, Balaki, usikie! Unisikilize, ewe mwana wa Sipori! Mungu si mutu, hata aseme uongo, wala si mwanadamu, hata abadilishe nia yake! Ataahidi kitu na asikifanye, au kusema kitu asikitimize? Nimepewa amri ya kubariki, naye amebariki wala siwezi kuigeuza. Yawe hajaona ubaya kwa watu wa Yakobo, wala uovu kwa hao watu wa Israeli. Yawe Mungu wao yuko pamoja nao, Yeye anasifiwa kwa vigelegele kati yao, yeye anapokea sifa zao za kifalme. Mungu aliyewatoa kutoka Misri, anawapigania kwa nguvu kama za mbogo. Hakika ulozi hauwezi kuwapinga watu wa Yakobo, wala uchawi juu ya watu wa Israeli. Sasa juu ya Israeli, watu watasema: Muangalie maajabu Mungu aliyotenda! Angalia! Waisraeli wameinuka kama simba dike, wanasimama kama simba dume. Ni kama simba asiyelala mpaka amalize windo lake, na kunywa damu ya windo. Halafu Balaki akamwambia Balamu: Basi, usiwalaani wala usiwabariki kabisa! Lakini Balamu akamujibu Balaki: Sikukuambia kwamba kile Yawe anachosema ndicho ninachopaswa kufanya? Balaki akamwambia Balamu: Kuja, nitakupeleka pahali pengine. Labda Mungu atakubali uwalaani watu hao kutoka huko kwa ajili yangu. Basi, Balaki akamupeleka Balamu mpaka kwenye kilele cha mulima Peori, ambapo mutu akisimama anaona katika jangwa. Balamu akamwambia Balaki: Unijengee mazabahu saba hapa, unitayarishie ngombe dume saba na kondoo dume saba. Balaki akafanya kama vile alivyoambiwa na Balamu, kisha akatoa juu ya kila mazabahu ngombe dume mumoja na kondoo dume mumoja. Sasa Balamu akatambua kwamba Yawe alipenda kuwabariki Waisraeli, kwa hiyo hakukwenda sawa vile mara ingine kwa kutafuta uchawi. Akaelekea kwenye jangwa, akainua macho, akawaona Waisraeli wamepiga kambi kila kabila pahali pake. Kisha Roho ya Mungu ikamufikia, naye akasema mashairi haya ya Yawe: Mashairi yangu mimi Balamu mwana wa Peori mashairi ya mutu aliyefumbuliwa macho. Anasema yeye aliyesikia maneno ya Mungu, mutu aliyeona maono ya Mungu Mwenye Nguvu, mutu anayeinama uso mpaka chini na kuona wazi. Hema zenu zinapendeza sana, enyi watu wa Yakobo; hakika, kambi zenu, enyi watu wa Israeli! Ni kama mabonde yanayotiririka maji, kama bustani kandokando ya muto, kama miti ya mishubiri Yawe aliyopanda, kama mierezi kandokando ya maji. Watakuwa na hazina ya kutosha ya maji, mbegu yao itapata maji mengi, mufalme wao atakuwa mukubwa kuliko Agagi, na ufalme wake utatukuka sana. Mungu aliwaondoa kutoka Misri, naye anawapigania kwa nguvu kama mbogo. Atayateketeza mataifa yanayokuwa waadui zao, atavunjavunja mifupa yao, atawachoma kwa mishale yake. Atavizia na kulala chini kama simba, nani atasubutu kumwamusha? Abarikiwe yeyote atakayekubariki wewe Israeli, alaaniwe yeyote atakayekulaani. Balaki akawaka hasira juu ya Balamu, akapiga mikono kwa kasirani na kumwambia: Nilikuita uwalaani waadui zangu, lakini mara hizi zote tatu umewabariki! Sasa! Kwenda zako. Nilikuwa nimekuahidi kukupa zawadi nyingi, lakini Yawe hakukujalia kupata zawadi hizo, amekunyima! Balamu akamujibu Balaki: Unakumbuka nilivyowaambia wajumbe uliowatuma kwangu. Niliwaambia kwamba hata kama ungenipa nyumba yako imejaa feza na zahabu, mimi sitaweza kubadilisha agizo la Yawe, kwa kufanya jambo lolote, jema au baya kwa mapenzi yangu mwenyewe. Nilisema kwamba atakachosema Yawe ndicho nitakachosema. Sasa ninarudi kwa watu wangu, lakini mbele sijaondoka, acha nikuambie mambo ambayo watu hao watawatendea watu wako siku zinazokuja. Basi, Balamu akasema mashairi haya: Mashairi yangu mimi Balamu mwana wa Beori, mashairi ya mutu aliyefumbuliwa macho, mashairi ya mutu aliyesikia maneno ya Mungu, na mutu anayejua maarifa ya Mungu Mukubwa, mutu anayeona maono ya Mungu Mwenye Nguvu, mutu anayeinama uso mpaka chini, macho wazi. Ninamwona atakayekuja, ninamwona, lakini hayuko karibu. Nyota itatokea kwa wazao wa Yakobo, atatokea mufalme kati ya Waisraeli. Kwa fimbo yake atapiga viongozi wa Wamoabu, atawaangamiza wazao wote wa Seti. Edomu itakuwa urizi wake, Seiri itakuwa mali yake, Israeli itapata ushindi mukubwa. Mumoja wa wazao wa Yakobo atatawala naye atawaangamiza watakaobaki katika muji. Kisha Balamu akawaangalia Waamaleki, akatoa mashairi haya: Amaleki ni taifa lenye nguvu kuliko yote, lakini kwa mwisho litaangamia kabisa. Kisha Balamu akawaangalia Wakeni, akatoa mashairi haya: Makao yenu ni salama, enyi Wakeni, kama chicha juu kabisa ya mulima. Lakini mutateketezwa, enyi Wakeni. Mutapelekwa mateka na Asuria mpaka wakati gani? Tena Balamu akatoa mashairi haya: Ole! Nani ataishi Mungu atakapofanya hayo? Mashua zitafika kutoka Kitimu, wataishambulia Asuria na Eberi, lakini nao vilevile wataangamia milele. Basi, Balamu akaondoka, akarudi kwake; Balaki vilevile akaenda zake. Waisraeli walipokuwa kule Sitimu, wanaume wakaanza kuzini na wanawake wa Moabu. Wanawake hao waliwaalika Waisraeli washiriki matambiko waliyotambikia miungu yao, nao Waisraeli wakakula chakula na kuabudu miungu yao. Ndivyo Waisraeli walivyojiunga na mungu Bali wa Peori, nayo hasira ya Yawe ikawaka juu yao. Basi, Yawe akamwambia Musa: Utwae viongozi wote wa Israeli, uwatundike mbele yangu jua kati, kusudi kasirani yangu juu yenu ipite. Musa akawaambia waamuzi wa Israeli: Kila mumoja wenu amwue mutu yeyote kati yenu ambaye amejiunga na mungu Bali wa Peori. Wakati huohuo mutu mumoja akamuleta mwanamuke mumoja Mumidiani katika nyumba yake, Musa na Waisraeli wote pamoja wakiwa wanaomboleza kwenye mulango wa hema la mukutano. Basi, Finehasi mwana wa Eleazari mujukuu wa kuhani Haruni alipoona hayo, akasimama, akatoka, akatwaa mukuki na kumufuatilia yule Mwisraeli mpaka ndani ya hema, akawachoma mukuki wote wawili ndani ya tumbo. Ugonjwa mukali uliokuwa umewaangamiza Waisraeli ukakomeshwa. Waliokufa kutokana na ugonjwa ule mukali walikuwa watu elfu makumi mbili na ine. Yawe akamwambia Musa: Finehasi mwana wa Eleazari, mujukuu wa kuhani Haruni, ameizuia hasira yangu juu ya Waisraeli; kati yenu ni yeye tu aliyeona wivu kama ule ninaokuwa nao mimi. Ndiyo maana sikuwaangamiza Waisraeli wote kwa hasira yangu. Kwa hiyo umwambie kwamba ninafanya naye agano la amani. Ninaagana naye kwamba yeye na wazao wake watakuwa makuhani milele kwa sababu aliona wivu kwa ajili yangu mimi Mungu wake, akawafanyia Waisraeli upatanisho. Huyo Mwisraeli aliyeuawa pamoja na mwanamuke wa Kimidiani aliitwa Zimuri mwana wa Salu, kiongozi wa jamaa moja katika kabila la Simeoni. Na huyo mwanamuke Mumidiani aliyeuawa aliitwa Kozibi binti ya Suri, aliyekuwa kiongozi wa ukoo fulani huko Midiani. Yawe akamwambia Musa: Uwachokoze Wamidiani na kuwaangamiza, kwa sababu waliwachokoza ninyi kwa werevu wao, ambao kwa njia yake wamewadanganya katika jambo la Peori, na kwa sababu ya Kozibi, binti yao, aliyeuawa wakati ugonjwa mukali ulipotokea kule Peori. Kisha ule ugonjwa, Yawe akamwambia Musa na Eleazari mwana wa kuhani Haruni. Muhesabu Waisraeli wote, kila mutu kufuatana na jamaa yake. Muwahesabu watu wote wenye umri wa miaka makumi mbili na zaidi wanaofaa kwenda katika jeshi. Musa na kuhani Eleazari wakazungumuza na watu kwenye inchi za mabonde za Moabu, ngambo ya muto Yordani, karibu na Yeriko, wakawaambia: Muhesabu watu kuanzia na wenye umri wa miaka makumi mbili na zaidi, kama vile Yawe alivyomwamuru Musa. Hesabu ya Waisraeli waliotoka Misri ni hii: Kwanza ni kabila la Rubeni, muzaliwa wa kwanza wa Yakobo. Hanoki, Palu, Hesironi na Karmi. Hizo ndizo ukoo za kabila la Rubeni. Hesabu ya wanaume waliohesabiwa ni elfu makumi ine na tatu, mia saba na makumi tatu. Wazao wa Palu walikuwa Eliabu, na wana wake Nemueli, Datani na Abiramu. Hawa wawili: Datani na Abiramu, ndio waliokuwa wamechaguliwa, lakini wakamupinga Musa na Haruni, na kujiunga na wafuasi wa Kora wakati walipomwasi Yawe. Wakati huo udongo ukafunguka ikawameza, wakakufa pamoja na Kora na wafuasi wake moto ulipoangamiza watu mia mbili makumi tano; wakakuwa onyo kwa watu. Pamoja na hayo wana wa Kora hawakukufa. Kabila la Simeoni. Nemueli, Yamini, Yakini, Zera na Sauli. Hizo ndizo ukoo za kabila la Simeoni, jumla yao wanaume elfu makumi mbili na mbili mia mbili. Kabila la Gadi lilikuwa na jamaa za Sefoni, Hagi, Suni, Ozini, Eri, Arodi na Areli. Hizo ndizo ukoo za kabila la Gadi, jumla wanaume elfu makumi ine mia tano. Kabila la Yuda lilikuwa na Eri na Onani. Hawa walikufia katika inchi ya Kanana. Kabila la Yuda lilikuwa na jamaa za Sela, Peresi, na Zera. Kutoka kwa Peresi, jamaa ya Hesironi na Hamuli. Hizo ndizo ukoo za Yuda, jumla wanaume elfu makumi saba na sita mia tano. Kabila la Isakari lilikuwa na jamaa za Tola, Puva, Yasubu na wa Simironi. Hizo ndizo ukoo za Isakari, jumla wanaume elfu makumi sita na ine mia tatu. Kabila la Zebuluni lilikuwa na jamaa za Seredi, wa Eloni na wa Yaleli. Hizo ndizo ukoo za Zebuluni, jumla wanaume elfu makumi sita mia tano. Kabila la Yosefu baba ya Manase na Efuraimu. Kabila la Manase lilikuwa na jamaa ya: Makiri, Gileadi, Yezeri, Heleki, Asirieli, Sekemu, Semida na Heferi. Selofehadi mwana wa Heferi hakupata watoto wanaume lakini wanawake tu, nao ni Mala, Noa, Hogula, Milka na Tirsa. Hizo ndizo ukoo za Manase, jumla wanaume elfu makumi tano na mbili mia saba. Kabila la Efuraimu lilikuwa na jamaa za Sutela, Bekeri na Tahani. Ukoo wa Erani ulikuwa na jamaa ya Sutela. Hizo ndizo ukoo za Efuraimu, jumla wanaume elfu makumi tatu na mbili mia tano. Zote hizo zilitokana na Yosefu. Kabila la Benjamina lilikuwa na jamaa za Bela, Asibeli, Ahiramu, Sufamu na Hufamu. Ukoo za Ardi na Namani, zilitokana na Bela. Hizo ndizo ukoo za Benjamina, jumla wanaume elfu makumi ine na tano mia sita. Kabila la Dani lilikuwa na jamaa ya Suhamu; ukoo ulikuwa na wanaume elfu makumi sita na ine mia ine. Kabila la Aseri lilikuwa na jamaa za Imuna, Isiwi na Beria. Ukoo za Heberi na Malkieli zilitokana na Beria. Aseri alikuwa na binti aliyeitwa Sera. Hizo ndizo ukoo za kabila la Aseri, jumla wanaume elfu makumi tano na tatu mia ine. Kabila la Nafutali lilikuwa na jamaa za Yaseli, Guni, Yeseri na Silemu. Hizi ndizo ukoo za kabila la Nafutali, jumla wanaume elfu makumi ine na tano mia ine. Hesabu ya wanaume Waisraeli waliohesabiwa ilikuwa elfu mia sita, na moja mia saba na makumi tatu. Kisha Yawe akamwambia Musa: Makabila haya yatagawanyiwa inchi ikuwe urizi wao, kulingana na hesabu ya majina yao. Kabila kubwa litapewa sehemu yao kubwa na dogo litapewa sehemu yao ndogo. Kila kabila litapewa urizi wake kulingana na hesabu ya watu wake. Hata hivyo ugawanyaji wa inchi utafanywa kwa kura. Kila kabila litarizi kulingana na majina ya ukoo wao. Urizi wa kila kabila utagawanywa kwa kura, kila kabila litapata kulingana na ukubwa au udogo wake. Hizi ndizo ukoo za Walawi zilizohesabiwa na jamaa zao Gersoni, Kohati na Merari, pamoja na jamaa za Libini, Hebroni, Mali, Musi na Kora. Kohati alikuwa baba ya Amuramu. Muke wa Amuramu aliitwa Yokebedi binti ya Lawi, aliyezaliwa Misri. Huyu alimuzalia Amuramu watoto wawili wanaume, Haruni na Musa, na binti mumoja, Miriamu. Haruni alikuwa na watoto wanaume wane, Nadabu, Abihu, Eleazari na Itamari. Nadabu na Abihu walikufa walipomutolea Yawe sadaka ya moto usiofaa. Hesabu ya Walawi wanaume wenye umri wa mwezi mumoja na zaidi ilikuwa elfu makumi mbili na tatu. Hawa hawakuhesabiwa pamoja na Waisraeli wengine kwa sababu wao hawakupewa urizi wowote kati yao. Hao ndio wanaume Waisraeli waliohesabiwa na Musa na kuhani Eleazari katika inchi za mabonde za Moabu, ngambo ya muto Yordani, karibu na Yeriko. Kati yao hakukuwa hata mutu mumoja aliyebakia kati ya wale waliohesabiwa na Musa na kuhani Haruni ambao walifanya hesabu ya kwanza katika jangwa la Sinai. Yawe alikuwa amesema kwamba wote watakufia katika jangwa, na kweli hakuna hata mumoja wao aliyebaki muzima, isipokuwa Kalebu mwana wa Yefune, na Yoshua mwana wa Nuni. Mala, Noa, Hogla, Milka na Tirsa walikuwa wabinti za Selofehadi. Naye Selofehadi alikuwa mwana wa Heferi mwana wa Gileadi mwana wa Makiri mwana wa Manase mwana wa Yosefu. Basi, hao wabinti wane wakamwendea Musa, wakasimama mbele yake na kuhani Eleazari na viongozi wote wa Waisraeli, kwenye mulango wa hema la mukutano, wakasema: Baba yetu alikufia katika jangwa na bila mutoto yeyote mwanaume. Yeye hakukuwa kati ya wafuasi wa Kora waliokusanyika mbele ya Yawe, lakini alikufa kutokana na zambi yake mwenyewe. Hakukuwa na mutoto mwanaume. Kwa nini basi jina la baba yetu lifutwe katika ukoo wake kwa sababu hakukuwa na mutoto mwanaume? Utupatie urizi pamoja na wandugu za baba yetu. Musa akaleta malalamiko yao mbele ya Yawe. Yawe akamwambia Musa: Wanachosema wabinti za Selofehadi ni kweli; uwape urizi pamoja na wandugu za baba yao, watwae urizi wake. Kisha uwaambie Waisraeli kwamba mutu yeyote akikufa bila kuacha mutoto mwanaume, urizi wake utapewa kwa binti yake. Ikiwa hana binti, basi urizi huo utapewa kwa wandugu zake wanaume. Na ikiwa hana ndugu mwanaume, basi urizi wake utawaendea baba zake wakubwa na wadogo. Na ikiwa baba yake hana ndugu mwanaume, basi urizi wake utamwendea wandugu zake wa karibu, naye ataurizi kama vile mali yake. Hii itakuwa sharti na agizo kwa Waisraeli, kama vile mimi Yawe nilivyokuamuru. Yawe akamwambia Musa: Panda juu ya mulima huu wa miinuko ya Abarimu uangalie inchi ambayo nimewapa Waisraeli. Ukisha kuiona, utakufa na kukutana na wazee wako, kama vile ndugu yako Haruni alivyokutana nao, kwa sababu hamukuitii amri yangu kule katika jangwa la Sini, wakati watu wote pamoja waliponigombanisha kule Meriba. Ninyi hamukuacha utukufu wangu uonekane mbele yao walipotaka wapewe maji. (Meriba ni chemichemi ya maji ya Kadesi katika jangwa la Sini). Naye Musa akamwomba Yawe: Ee Yawe, Mungu unayekuwa asili ya uzima wote, ninakuomba umuchague mutu wa kusimamia watu hawa, ambaye atawatangulia na kuwaongoza katika shuguli zao zote, kusudi wasikuwe kama kondoo wasiokuwa na muchungaji. Yawe akamwambia Musa: Umutwae Yoshua mwana wa Nuni, mutu mwenye roho nzuri, kisha uweke mikono juu yake, na kumusimamisha mbele ya kuhani Eleazari na watu wote, umupatie kazi hiyo. Umupe sehemu ya mamlaka yako kusudi Waisraeli wote wamutii. Yeye atamutegemea kuhani Eleazari ambaye atamujulisha mapenzi yangu kwa kutumia jiwe la shauri. Kwa njia hii, Eleazari atamwongoza Yoshua na Waisraeli wote wanapotoka na wanapoingia. Musa akafanya kama vile alivyoamriwa na Yawe. Akamutwaa Yoshua na kumusimamisha mbele ya kuhani Eleazari na Waisraeli wote. Kisha akamwekea mikono juu ya kichwa na kumupa mamlaka kama vile alivyoagizwa na Yawe. Yawe akamwambia Musa: Uwaamuru Waisraeli maneno haya: Ninyi mutanitolea kwa wakati wake sadaka zinazotakiwa: vyakula vya kuteketezwa kwa moto, vyenye harufu nzuri ya kupendeza. Uwaambie kwamba sadaka watakayonitolea ya kuteketezwa kwa moto, itakuwa hii: wana-kondoo wawili wa mwaka mumoja wasiokuwa na kilema chochote, kwa ajili ya sadaka ya kuteketezwa ya kila siku. Mwana-kondoo mumoja atatolewa asubui na wa pili magaribi; kila mumoja atatolewa pamoja na sadaka ya vyakula ya kilo moja ya unga uliochanganywa pamoja na litre moja ya mafuta bora yaliyopondwa. Hii ni sadaka ya kutolewa kila siku inayoteketezwa kabisa kwa moto, ambayo ilitolewa kwa mara ya kwanza kwenye mulima Sinai kama sadaka ya ngano, harufu nzuri ya kumupendeza Yawe. Sadaka ya kinywaji itakayotolewa na kila mwana-kondoo ni litre moja ya divai. Utaimimina sadaka hii ya kinywaji kikali Pahali Patakatifu. Wakati wa magaribi utamutoa yule mwana-kondoo mwingine kwa kuteketezwa kwa moto, pamoja na sadaka zile za ngano na za kinywaji. Itakuwa sadaka yenye harufu nzuri ya kumupendeza Yawe. Siku ya Sabato, mutatoa sadaka ya wana-kondoo dume wawili wa mwaka mumoja wasiokuwa na kilema, sadaka ya vyakula ya kilo mbili za unga laini uliochanganywa na mafuta, na sadaka yake ya kinywaji. Sadaka hii ya kuteketezwa itatolewa kila siku ya Sabato zaidi ya ile sadaka ya kila siku pamoja na sadaka yake ya kinywaji. Kwa mwanzo wa kila mwezi, mutamutolea Yawe sadaka ya kuteketezwa: wana-ngombe dume wawili, kondoo dume mumoja, wana-kondoo dume saba wa mwaka mumoja, wasiokuwa na kilema. Mutatoa sadaka ya vyakula ya unga laini kilo tatu, uliochanganywa na mafuta kwa kila ngombe dume mumoja; mutatoa kilo mbili za unga; kwa kila kondoo dume, na kilo moja ya unga kwa kila mwana-kondoo. Sadaka hizi za kuteketezwa ni sadaka za chakula zenye harufu ya kumupendeza Yawe. Kipimo cha sadaka ya kinywaji kinachohitajika ni litre mbili za divai kwa kila ngombe dume; litre moja na nusu kwa kila kondoo dume, na litre moja kwa kila mwana-kondoo. Hii ndiyo sadaka ya kuteketezwa ya kila mwezi katika mwaka muzima. Tena mutamutolea Yawe sadaka kwa ajili ya zambi, beberu mumoja, zaidi ya ile sadaka ya kuteketezwa ya kila siku na sadaka yake ya kinywaji. Siku ya kumi na ine ya mwezi wa kwanza ni Pasaka ya Yawe. Siku ya kumi na tano ya mwezi huohuo ni sikukuu. Kwa muda wa siku saba mutakula mikate isiyotiwa chachu. Katika siku ya kwanza kutakuwa mukutano mutakatifu. Siku hiyo hamutafanya kazi. Mutatoa sadaka ya kuteketezwa kama vile sadaka ya ngano kwa Yawe: wana-ngombe dume wawili, kondoo dume mumoja, wana-kondoo dume saba wa mwaka mumoja, wote wakuwe bila kilema. Sadaka ya ngano itakayoandamana nazo itakuwa ya unga safi uliochanganywa na mafuta, kilo tatu kwa kila ngombe dume, kilo mbili kwa kila kondoo dume, na kilo moja kwa kila mumoja wa wale wana-kondoo saba. Mutatoa vilevile beberu mumoja kuwa sadaka kwa ajili ya zambi kwa kuwafanyia upatanisho. Mutatolea vitu hivi zaidi ya ile sadaka ya kuteketezwa ya kawaida inayotolewa kila siku asubui. Vivyo hivyo, kwa muda wa siku saba, mutatoa kila siku sadaka ya ngano ya kuteketezwa. Itakuwa ni harufu nzuri ya kumupendeza Yawe. Hii mutaitoa zaidi ya ile sadaka ya kuteketezwa ya kila siku na sadaka yake ya kinywaji. Katika siku ya saba mutafanya mukutano mutakatifu; musifanye kazi. Katika siku ya kwanza ya sikukuu ya majuma wakati munapomutolea Yawe malimbuko ya ngano zenu, mutafanya mukutano mutakatifu; musifanye kazi. Mutatoa sadaka ya kuteketezwa, harufu nzuri ya kumupendeza Yawe: wana-ngombe dume wawili, kondoo dume mumoja, na wana-kondoo dume saba wa mwaka mumoja, wote hao wakuwe bila kilema. Sadaka ya ngano itakayoandamana nazo itakuwa ya unga safi uliochanganywa na mafuta kilo tatu kwa kila ngombe dume, kilo mbili kwa kila kondoo dume, na kilo moja kwa kila mwana-kondoo. Mutatoa vilevile beberu mumoja kuwa sadaka kwa ajili ya zambi kwa kuwafanyia upatanisho. Mutatoa vitu hivi zaidi ya ile sadaka ya kuteketezwa ya kawaida pamoja na sadaka yake ya kinywaji. Siku ya kwanza ya mwezi wa saba, mutafanya mukutano mutakatifu. Musifanye kazi. Hiyo ni siku ya kupiga baragumu. Mutatoa sadaka ya kuteketezwa, harufu nzuri ya kumupendeza Yawe: wana-ngombe dume wawili, kondoo dume wawili, na wana-kondoo dume saba wa mwaka mumoja, wote wakuwe wasiokuwa na kilema chochote. Mutatoa vilevile sadaka yake ya vyakula ya unga safi uliochanganywa na mafuta: kilo tatu kwa kila ngombe dume, kilo mbili kwa kila kondoo dume, na kilo moja kwa kila mwana-kondoo. Tena mutatoa beberu mumoja kuwa sadaka kwa ajili ya zambi kwa kuwafanyia upatanisho. Mutatoa vitu hivi zaidi ya ile sadaka ya kuteketezwa ya mwezi mupya na sadaka yake ya vyakula, na sadaka ya kila siku ya kuteketezwa pamoja na sadaka yake ya vyakula na sadaka zake za kinywaji kama vile inavyoagizwa. Itakuwa harufu nzuri yenye kupendeza; ni sadaka kwa Yawe iliyoteketezwa kwa moto. Siku ya kumi ya mwezi wa saba mutafanya mukutano mutakatifu. Siku hiyo munapaswa kufunga kula na musifanye kazi. Mutamutolea Yawe sadaka ya kuteketezwa kwa moto, harufu ya kumupendeza Yawe: mwana-ngombe mumoja, kondoo dume mumoja, wana-kondoo saba wa mwaka mumoja. Wote wasikuwe na kilema. Zaidi ya vitu hivi mutatoa sadaka ya unga safi uliochanganywa na mafuta kilo tatu pamoja na huyo ngombe dume, kilo mbili pamoja na yule kondoo dume, na kilo moja kwa kila mwana-kondoo. Mutatoa vilevile beberu mumoja kwa sadaka kwa ajili ya zambi zaidi ya sadaka ya kufanyiwa upatanisho, pamoja na sadaka ya kawaida ya kuteketezwa na sadaka yake ya vyakula na sadaka zake za kinywaji. Siku ya kumi na tano ya mwezi wa saba, mutafanya mukutano mutakatifu. Hamutafanya kazi siku hiyo. Mutafanya sikukuu kwa ajili ya Yawe kwa siku saba. Mutatoa sadaka ya kuteketezwa kwa moto, yenye harufu nzuri inayomupendeza Yawe: wana-ngombe dume kumi na watatu, kondoo dume wawili, wana-kondoo kumi na wane wa mwaka mumoja. Wote wasikuwe na kilema. Sadaka itakayoandamana nazo itakuwa unga safi uliochanganywa na mafuta: kilo tatu kwa kila ngombe dume, kilo mbili kwa kila kondoo, na kilo moja kwa kila mwana-kondoo. Mutatoa vilevile beberu mumoja kuwa sadaka kwa ajili ya zambi, zaidi ya ile sadaka ya kawaida ya kuteketezwa, pamoja na sadaka yake ya vyakula na sadaka yake ya kinywaji. Siku ya pili mutatoa: wana-ngombe dume kumi na wawili, kondoo dume wawili, wana-kondoo dume kumi na wane, wa mwaka mumoja wasiokuwa na kilema. Mutatoa vilevile sadaka ya vyakula na sadaka za vinywaji pamoja na wale wana-ngombe dume, kondoo na wana-kondoo, kulingana na hesabu yao, kama vile inavyoagizwa. Mutatoa vilevile beberu mumoja kuwa sadaka kwa ajili ya zambi, zaidi ya sadaka ya kuteketezwa ya kawaida pamoja na sadaka yake ya vyakula na sadaka yake ya kinywaji. Siku ya tatu mutatoa: ngombe dume kumi na mumoja, kondoo wawili, wana-kondoo kumi na wane wa mwaka mumoja, wasiokuwa na kilema. Mutawatolea pamoja na sadaka ya vyakula na sadaka za kinywaji kulingana na hesabu yao, kama vile inavyoagizwa. Vilevile mutatoa beberu mumoja kuwa sadaka kwa ajili ya zambi, zaidi ya ile sadaka ya kawaida ya kuteketezwa pamoja na sadaka yake ya vyakula na sadaka yake ya kinywaji. Siku ya ine mutatoa: ngombe dume kumi, kondoo dume wawili, wana-kondoo dume kumi na wane, wasiokuwa na kilema. Mutatoa vilevile sadaka ya vyakula na sadaka za kinywaji pamoja na hao ngombe dume na kondoo na wana-kondoo kulingana na hesabu yao, kama vile inavyoagizwa. Mutatoa vilevile beberu mumoja kuwa sadaka kwa ajili ya zambi zaidi ya sadaka ya kawaida ya kuteketezwa, pamoja na sadaka yake ya vyakula na sadaka yake ya kinywaji. Siku ya tano, mutatoa ngombe dume tisa, kondoo wawili, wana-kondoo dume kumi na wane wa mwaka mumoja wasiokuwa na kilema. Mutatoa vilevile sadaka ya vyakula na sadaka za kinywaji pamoja na hao ngombe dume na kondoo na wana-kondoo kulingana na hesabu yao, kama vile inavyoagizwa. Mutatoa vilevile beberu mumoja kuwa sadaka kwa ajili ya zambi, zaidi ya sadaka ya kawaida ya kuteketezwa, pamoja na sadaka yake ya vyakula na sadaka yake ya kinywaji. Siku ya sita mutatoa ngombe dume wanane, kondoo dume wawili, wana-kondoo dume kumi na wane wa mwaka mumoja wasiokuwa na kilema. Mutatoa vilevile sadaka ya vyakula na sadaka za kinywaji pamoja na hao ngombe dume, kondoo dume na wana-kondoo kulingana na hesabu yao, kama vile inavyoagizwa. Mutatoa vilevile beberu mumoja kuwa sadaka kwa ajili ya zambi, pamoja na sadaka yake ya vyakula na sadaka zake za kinywaji. Siku ya saba mutatoa ngombe dume saba, kondoo dume watatu, wana-kondoo dume kumi na wane wa mwaka mumoja, wasiokuwa na kilema. Mutatoa vilevile sadaka ya vyakula na sadaka za kinywaji pamoja na hao ngombe dume, kondoo dume, na wana-kondoo, kulingana na hesabu yao, kama vile inavyoagizwa. Mutatoa vilevile beberu mumoja kuwa sadaka kwa ajili ya zambi, zaidi ya ile sadaka ya kawaida ya kuteketezwa, pamoja na sadaka yake ya vyakula na sadaka yake ya kinywaji. Siku ya nane mutakuwa na mukutano mutakatifu. Musifanye kazi siku hiyo. Mutatoa sadaka ya kuteketezwa yenye harufu nzuri inayomupendeza Yawe: ngombe dume mumoja, kondoo dume mumoja, na wana-kondoo dume saba wa mwaka mumoja wasiokuwa na kilema. Mutatoa vilevile sadaka ya vyakula na sadaka za kinywaji pamoja na huyo ngombe dume, huyo kondoo dume, na wale wana-kondoo kulingana na hesabu yao kama vile inavyoagizwa. Vilevile mutatoa beberu mumoja kuwa sadaka kwa ajili ya zambi, zaidi ya ile sadaka ya kawaida ya kuteketezwa pamoja na sadaka yake ya vyakula na sadaka ya kinywaji. Haya ndiyo maagizo juu ya sadaka mutakazomutolea Yawe wakati wa sikukuu zenu zilizopangwa. Zaidi ya hizi zote, kuna vilevile sadaka za kuteketezwa, za vyakula na za kinywaji, za kutimiza kiapo na za mapenzi, na za amani. Basi, Musa akawaambia Waisraeli kila kitu kama vile Yawe alivyomwamuru. Kisha Musa akazungumuza na viongozi wa makabila ya Israeli, akawaambia: Hili ndilo neno lililoamriwa na Yawe: Mutu akiahidi mbele ya Yawe au akifanya kiapo, anapaswa kutimiza ahadi yake. Anapaswa kushika yale yote aliyotamka kwa kinywa chake. Binti ambaye angali anaishi katika nyumba ya baba yake akiahidi mbele ya Yawe na kufanya kiapo, na baba yake akisikia ahadi hiyo naye hamupingi, yule binti atafungwa na kila kiapo na ahadi aliyofanya. Lakini kama baba yake akisikia juu ya kiapo hicho, akimupinga, basi kiapo chake au ahadi yake havitamufunga. Yawe atamusamehe kwa sababu baba yake amelipinga jambo hilo. Ikiwa binti ataolewa kisha kufanya kiapo au kuahidi bila kufikiri vizuri kwanza, halafu mume wake akisikia jambo hilo naye hamupingi, muke wake atafungwa na kila kiapo au ahadi aliyofanya. Lakini kama mume wake akisikia jambo hilo, akimupinga, basi huyo mume wake atavunja kiapo cha muke wake na maneno yale aliyosema bila kufikiri; naye Yawe atamusamehe. Lakini kiapo au ahadi yoyote mujane aliyoweka au mwanamuke aliyeachana na mume wake ambayo kwa njia yake amejifunga, inapaswa kumufunga. Mwanamuke aliyeolewa akifanya ahadi au kiapo akiwa katika nyumba ya mume wake, kisha mume wake akisikia jambo hilo naye hamupingi, wala kumwambia kitu, basi, viapo vyake vyote vitamufunga; vilevile na ahadi zake zote zitamufunga. Lakini kama mume wake atakaposikia habari zake, akizifunga na kuzivunja, basi, hata kama alitaka kutimiza kiapo au ahadi zake, hataombwa kuzitimiza. Mume wake atakuwa amezifunga na Yawe atamusamehe. Mume wake anaweza kuhakikisha au kufunga kiapo au ahadi yoyote inayomufunga. Lakini ikiwa mume wake hatasema neno lolote tangu siku atakaposikia habari za kiapo au ahadi ya muke wake, basi atakuwa ameihakikisha siku hiyo alipopata habari yake kwa sababu hakusema chochote. Lakini akiifunga na kuivunja muda fulani nyuma ya kusikia habari yake, basi yeye atabeba lazima ya kosa la muke wake. Haya ndiyo masharti ambayo Yawe alimwagiza Musa kati ya mume na muke wake, baba na binti yake, huyo binti akiwa bado kijana na anakaa katika nyumba ya baba yake. Yawe akasema na Musa, akamwambia: Uwalipize kisasi Wamidiani mambo waliyowatendea Waisraeli; kisha wewe utakufa. Basi Musa akazungumuza na watu akawaambia: Mutayarishe watu kwa vita waende kuwashambulia Wamidiani kwa kumulipizia Yawe kisasi. Kutoka kila kabila la Israeli, mutapeleka watu elfu moja kwa vita. Basi, watu elfu moja walitolewa kutoka kila kabila kati ya maelfu ya Waisraeli, jumla wanaume elfu kumi na mbili wenye silaha. Musa akawapeleka kwa vita chini ya uongozi wa Finehasi mwana wa kuhani Eleazari, akiwa na vyombo vya Pahali Patakatifu na baragumu za kutoa kitambulisho. Wakashambulia inchi ya Midiani, kama vile Yawe alivyomwamuru Musa, wakawaua wanaume wote. Kati ya watu hao waliouawa, kulikuwa wafalme watano wa Midiani: Ewi, Rekemu, Suri, Huri na Reba. Vilevile wakamwua Balamu mwana wa Beori. Waisraeli wakawapeleka kuwa wafungwa wanawake wa Midiani na watoto wao. Wakanyanganya: ngombe, kondoo na mali yao yote. Miji yao yote, makao yao na kambi zao zote wakaziteketeza kwa moto. Wakabeba vitu vyote walivyonyanganya na vile vyote walivyoteka na watu na ya nyama, wakamupelekea Musa na Eleazari, na Waisraeli wote waliokuwa katika kambi katika inchi za mabonde za Moabu, ngambo ya Yordani karibu na Yeriko. Musa, kuhani Eleazari, na viongozi wote wa Waisraeli wakatoka katika kambi, wakaenda kupokea waaskari. Musa akakasirikishwa na wakubwa wa jeshi na majemadari waliosimamia makundi ya waaskari elfu na makundi ya waaskari mamia waliorudi kutoka katika vita. Musa akawauliza: Kwa nini mumewaacha wanawake hawa wote wazima? Mukumbuke kwamba wanawake ndio waliofuata shauri la Balamu, wakasababisha Waisraeli wamwasi Yawe kule Peori hata ugonjwa mukali ukawafikia watu wa Yawe. Kwa hiyo basi, muwaue hawa watoto wote wanaume na kila mwanamuke kati yao aliyekwisha kulala na mwanaume. Lakini musiwaue wabinti wote ambao hawajapata kulala na mwanaume; muwaache wazima kwa ajili yenu wenyewe. Wote wale wanaokuwa kati yenu ambao wameua mutu au kugusa maiti wanapaswa kukaa inje ya kambi kwa muda wa siku saba; mujitakase pamoja na mateka wenu katika siku ya tatu na ya saba. Munapaswa kutakasa vilevile kila nguo, kila kitu kilichotengenezwa kwa ngozi, kwa manyoya ya kondoo au kwa muti. Kuhani Eleazari akawaambia wanaume waliorudi toka kwa vita: Hii ndiyo sheria ambayo Yawe amemupa Musa. Zahabu, feza, shaba, chuma, manjanja na madini ya risasi, ni kusema vitu vyote ambavyo vinavyovumilia moto, vitatakaswa kwa kupitishwa ndani ya moto. Hata hivyo, vinapaswa kutakaswa kwa maji ya utakaso. Vitu vingine vyote ambavyo haviwezi kuvumilia moto vitatakaswa kwa maji ya utakaso. Siku ya saba munapaswa kufua nguo zenu; ndipo mutakapokuwa safi na kuruhusiwa kuingia katika kambi. Yawe akasema na Musa, akamwambia: Wewe na kuhani Eleazari, pamoja na viongozi wa ukoo wa Waisraeli, mufanye hesabu ya vitu vilivyonyanganywa, watu na nyama. Mugawanye vitu katika mafungu mawili, fungu moja la waaskari waliokwenda kwa vita na fungu lingine kwa ajili ya watu wote wengine. Kisha kutokana na lile fungu la waaskari waliokwenda kwa vita, tenga sehemu ya kumi kwa ajili ya Yawe: kitu kimoja kutoka kila vitu mia tano, ikuwe ni watu, ngombe, punda, kondoo au mbuzi, umupe kuhani Eleazari kuwa sadaka kwa Yawe. Kutoka katika lile fungu la jamii nzima, utwae mumoja kati ya kila makumi tano, ikuwe ni watu, ngombe, punda, kondoo na mbuzi. Hivyo utawapa Walawi ambao wanashugulika na kazi katika hema la Yawe. Musa na kuhani Eleazari wakafanya kama vile Yawe alivyomwamuru Musa. Vitu watu waliotoka kwa vita walivyonyanganya vilikuwa: kondoo elfu mia sita na makumi saba na tano, ngombe elfu makumi saba na mbili, punda elfu makumi sita na moja, na wabinti elfu makumi tatu na mbili ambao hawakukuwa wamelala na mwanaume. Nusu yake, sehemu ambayo iligawanyiwa kwa waaskari waliokwenda kwa vita, ilikuwa kondoo elfu mia tatu makumi tatu na saba na mia tano, katika hao mia sita makumi saba na watano walitolewa kwa Yawe. Ngombe wa waaskari walikuwa elfu makumi tatu na sita, na katika hao makumi saba na wawili walitolewa sehemu ya kumi kwa Yawe. Punda wao walikuwa elfu makumi tatu mia tano, na katika hao makumi sita na mumoja walitolewa sehemu ya kumi kwa Yawe. Watu walikuwa elfu kumi na sita, na katika hao sehemu ya Yawe ilikuwa ni watu makumi tatu na wawili. Basi, Musa akamupa kuhani Eleazari sehemu ya kumi hiyo iliyotolewa kwa Yawe, kama vile Yawe alivyomwamuru Musa. Ile nusu Waisraeli waliyopewa, ambayo Musa alitenga na ile nusu waaskari waliokwenda kwa vita waliyopewa, ilikuwa kondoo elfu mia tatu na makumi tatu na saba na mia tano, ngombe elfu makumi tatu na sita, punda elfu makumi tatu na mia tano, na watu elfu kumi na sita. Kutoka nusu hii Waisraeli waliyopewa, Musa alitwaa mumoja kati ya kila mateka makumi tano na nyama makumi tano, kama alivyoamriwa na Yawe, akawapa Walawi ambao walitumika katika hema la Yawe. Kisha wakubwa wa majeshi, makapiteni na majemadari wa jeshi wakamwendea Musa wakamwambia: Sisi watumishi wako tumewahesabu waaskari wote wanaokuwa chini yetu na tumeona kwamba hakuna hata mumoja wao anayekosekana. Basi, tumeleta vyombo vya zahabu, mikufu, vikomo, pete za muhuri, pete za masikio na ushanga ambavyo kila mutu alipata. Tumevitoa kusudi nafsi zetu zifanyiwe upatanisho mbele ya Yawe. Musa na kuhani Eleazari wakapokea vitu vyote vilivyopambwa kwa zahabu. Jumla ya zahabu yote waliyomutolea Yawe ilikuwa karibu kilo mia mbili. (Kila askari alijitwalia vitu vyake mwenyewe). Basi, Musa na kuhani Eleazari wakapokea zahabu hiyo kutoka kwa majemadari wakaipeleka katika hema la mukutano, ikuwe ukumbusho wa Waisraeli mbele ya Yawe. Makabila ya Rubeni na Gadi yalikuwa na mifugo mingi sana. Basi, walipoona kwamba eneo la Yazeri na Gileadi lilifaa kwa mifugo, wakawaendea Musa, kuhani Eleazari na viongozi wa Waisraeli, wakawaambia: Miji ya Ataroti, Diboni, Yazeri, Nimura, Hesiboni, Eleale, Sebamu, Nebo na Beoni, inchi ambayo Yawe alishinda kwa ajili ya Waisraeli, ni inchi nzuri kwa mifugo, nasi tuko na mifugo mingi sana. Basi, kama tumepata kukubaliwa mbele yako, wewe Musa, tunakuomba utupatie inchi hii ikuwe mali yetu; usituvukishe ngambo ya muto Yordani. Musa akawajibu watu wa makabila ya Gadi na Rubeni: Munataka kubaki hapa wakati wandugu zenu Waisraeli wanakwenda kwa vita? Mbona munawavunja moyo Waisraeli wasiende katika inchi ambayo Yawe amewapa? Hivi ndivyo walivyofanya babu zenu nilipowatuma kutoka Kadesi-Barnea kwa kupeleleza inchi. Wao walikwenda mpaka bonde la Eskoli, wakaiona inchi, lakini waliporudi, wakavunja Waisraeli moyo kusudi wasiingie katika inchi Yawe aliyowapa. Yawe akawaka hasira siku hiyo, akaapa akisema: Hakika hakuna mutu yeyote kati ya watu waliotoka Misri mwenye umri wa miaka makumi mbili na zaidi atakayeona inchi niliyoapa kuwapa Abrahamu, Isaka na Yakobo, kwa sababu hawakunitii kwa ukamilifu. Wote hawataiona, isipokuwa Kalebu mwana wa Yefune wa ukoo wa Kenizi na Yoshua mwana wa Nuni, maana wao wamenitii kwa ukamilifu. Yawe akawaka hasira juu ya Waisraeli, akawafanya watangetange katika jangwa kwa muda wa miaka makumi ine; kizazi kizima kilichokuwa kimefanya maovu mbele yake kikakufa. Na sasa, enyi kizazi cha wenye zambi, mumesimama kwa pahali pa wazee wenu, kuongeza tena hasira kali ya Yawe juu ya Waisraeli. Kama ninyi mukikataa kumufuata, yeye atawaachilia tena katika jangwa, nanyi mutasababisha watu hawa wote waangamie. Basi, wakamwendea Musa, wakamwambia: Kwanza uturuhusu tuwajengee kondoo wetu mazizi, na watoto wetu miji hapa. Lakini sisi wenyewe tutatwaa silaha zetu tayari kwenda kwa vita pamoja na wandugu zetu Waisraeli, na tutakuwa kwa mustari wa mbele katika vita mpaka tuwafikishe pahali watakapokaa. Wakati huo watoto wetu watakaa kwenye miji yenye kuta, kwa kujilinda na wenyeji wa inchi hii. Hatutarudi kwenye nyumba mpaka pale Waisraeli wengine wote watakaporizi maeneo yao waliyogawanyiwa. Hatutarizi mali yoyote kati yao ngambo ya muto Yordani, kwa sababu sisi tumepata maeneo yetu ngambo hii, upande wa mashariki wa muto Yordani. Musa akawaambia: Kama kweli mutafanya kama vile mulivyosema, basi hapahapa mbele ya Yawe, mutwae silaha zenu kwenda kwa vita. Kila mupiganaji wenu atavuka muto Yordani na mukiwa chini ya uongozi wa Yawe, mutawashambulia waadui zetu mpaka Yawe awashinde, na kurizi inchi. Mukisha kufanya hayo, mutarudi, maana mutakuwa bila kosa mbele ya Yawe na wandugu zenu Waisraeli. Kisha Yawe atakubali inchi hii ya upande wa mashariki wa Yordani kuwa mali yenu. Lakini ninawaonya kwamba musipotimiza ahadi yenu, mutakuwa mumemutendea Yawe zambi; mujue kwa hakika kwamba mutaazibiwa. Muwajengee watoto wenu miji na kondoo wenu mazizi; lakini mufanye kama vile mulivyoahidi. Kisha, watu wa Gadi na wa Rubeni wakamwambia Musa: Sisi watumishi wako tutafanya kama vile ulivyotuamuru. Wake zetu, watoto wetu na kondoo na ngombe, watabaki hapa katika miji ya Gileadi. Lakini sisi watumishi wako tuko tayari kwenda kwa vita chini ya uongozi wa Yawe. Tutavuka muto Yordani na kupigana, kama vile ulivyosema. Basi, Musa akatoa amri hizi kwa kuhani Eleazari, kwa Yoshua mwana wa Nuni, na kwa viongozi wa jamaa za makabila ya Waisraeli: Ikiwa watu wa Gadi na wa Rubeni watavuka muto Yordani pamoja nanyi wakiwa na silaha zao chini ya uongozi wa Yawe, mukishinda na kuitwaa inchi hiyo, basi mutawapa inchi ya Gileadi ikuwe mali yao. Lakini kama hawatavuka muto Yordani pamoja nanyi na silaha zao, basi watarizi sehemu ya inchi ya Kanana pamoja nanyi. Watu wa Gadi na wa Rubeni wakajibu: Bwana, sisi tutafanya kama vile Yawe alivyotuambia sisi watumishi wako. Chini ya uongozi wa Yawe, tutavuka na silaha zetu mpaka katika inchi ya Kanana, lakini inchi tuliyopewa hapa upande wa mashariki wa Yordani itakuwa mali yetu. Basi, Musa akawapa watu wa makabila ya Gadi na Rubeni na nusu ya kabila la Manase mwana wa Yosefu, inchi yote ya mufalme Sihoni wa Waamori na inchi ya mufalme Ogi wa Basani pamoja na miji na maeneo yaliyokuwa kandokando ya miji hiyo. Kabila la Rubeni likaijenga miji ya Diboni, Ataroti, Aroeri, Aturoti-Sofani, Yazeri, Yogibeha, Beti-Nimira na Beti-Harani, miji yenye kuta na mazizi ya kondoo. Kabila la Gadi likajenga miji ya Hesiboni, Eleale, Kiriataimu, Nebo na Bali-Meoni (majina ya hiyo miji yalibadilishwa), na Sibuma. Miji waliyoijenga wakaipa majina mengine. Wazao wa Makiri mwana wa Manase wakashambulia inchi ya Gileadi, wakaiteka na kuwafukuza Waamori waliokuwa wanakaa mule. Kwa hiyo, Musa akawapa watu wa ukoo wa Makiri mwana wa Manase, inchi ya Gileadi, nao wakakaa mule. Yairi, wa kabila la Manase, akashambulia vijiji vya Gileadi na kuviteka, akavipa jina “Vijiji vya Yairi”. Naye Noba akashambulia na kuteka Kenati na vijiji vyake, akauita Noba, jina lake mwenyewe. Hivi ndivyo vituo ambavyo Waisraeli wakapiga kambi walipotoka Misri wakiwa katika makundi ya makabila yao chini ya uongozi wa Musa na Haruni. Musa aliandika jina la kila pahali walipopiga kambi, kituo kwa kituo, kwa agizo la Yawe. Waisraeli wakaondoka katika muji wa Ramesesi katika siku ya kumi na tano ya mwezi wa kwanza, siku moja nyuma ya Pasaka ya kwanza. Wakaondoka kwa uhodari mukubwa mbele ya Wamisri wote, ambao walikuwa wanazika wazaliwa wao wa kwanza wanaume Yawe aliowaua; maana Yawe alikuwa ameiazibu hata miungu yao. Basi, Waisraeli wakaondoka Ramesesi, wakapiga kambi yao huko Sukoti. Kutoka Sukoti, wakapiga kambi yao huko Etamu, kwenye ukingo wa jangwa. Kutoka Etamu, waligeuka na kurudi mpaka Pi-Hahiroti, upande wa mashariki wa Bali-Sefoni, wakapiga kambi yao karibu na Migidoli. Wakaondoka Pi-Hahiroti, wakapita bahari Nyekundu mpaka jangwa la Etamu; wakasafiri katika jangwa mwendo wa siku tatu, wakapiga kambi yao Mara. Kutoka Mara, wakasafiri mpaka Elimu; huko Elimu kulikuwa na chemichemi kumi na mbili za maji na mingazi makumi saba, wakapiga kambi yao pahali pale. Wakasafiri kutoka Elimu, wakapiga kambi yao karibu na bahari ya Nyekundu. Kutoka bahari Nyekundu wakapiga kambi yao katika jangwa la Sini. Kutoka jangwa la Sini, wakapiga kambi yao Dofuka. Kutoka Dofuka wakapiga kambi yao huko Alusi. Kutoka Alusi wakapiga kambi yao huko Refidimu, ambapo hapakukuwa maji ya kunywa. Wakaondoka Refidimu wakapiga kambi yao katika jangwa la Sinai. Kutoka Sinai wakapiga kambi yao huko Kibroti-Hatawa. Kutoka Kibroti-Hatawa, wakapiga kambi yao huko Haseroti. Kutoka Haseroti, wakapiga kambi yao huko Ritima. Kutoka Ritima, wakapiga kambi yao huko Rimoni-Perezi. Kutoka Rimoni-Perezi, wakapiga kambi yao huko Libuna. Kutoka Libuna wakapiga kambi yao Risa. Waliondoka Risa, wakapiga kambi yao huko Kehelata. Kutoka Kehelata, wakapiga kambi yao kwenye mulima Seferi. Kutoka mulima Seferi wakapiga kambi yao huko Harada. Kutoka Harada, wakapiga kambi yao huko Makeloti. Kutoka Makeloti, wakapiga kambi yao huko Tahati. Kutoka Tahati wakapiga kambi yao Tera. Kutoka Tera wakapiga kambi yao Mitika. Kutoka Mitika, wakapiga kambi yao Hasimona. Kutoka Hasimona, wakapiga kambi yao Musaroti. Kutoka Musaroti, wakapiga kambi yao Bene-Yaakani. Kutoka Bene-Yaakani, wakapiga kambi yao Hori-Hagidigadi. Kutoka Hori-Hagidigadi, wakapiga kambi yao Yotibata. Kutoka Yotibata, wakapiga kambi yao Abarona. Kutoka Abarona, wakapiga kambi yao Esioni-Geberi. Waliondoka Esioni-Geberi, wakasafiri na kupiga kambi yao katika jangwa la Sini, ni kusema Kadesi. Kutoka Kadesi, wakapiga kambi yao juu ya mulima Hori, kwenye mupaka wa inchi ya Edomu. Kwa agizo la Yawe kuhani Haruni akapanda juu ya mulima Hori, na huko, akakufa katika siku ya kwanza ya mwezi wa tano, mwaka wa makumi ine tangu Waisraeli walipotoka katika inchi ya Misri. Haruni alikuwa na umri wa miaka mia moja makumi mbili na mitatu alipokufa juu ya mulima Hori. Mufalme wa Aradi, Mukanana, aliyekaa Negebu katika inchi ya Kanana akapata habari kwamba Waisraeli walikuwa wanakuja. Kutoka mulima Hori, Waisraeli wakapiga kambi yao Salmona. Kutoka Salmona, wakapiga kambi yao Punoni. Kutoka Punoni, wakapiga kambi yao Oboti. Kutoka Oboti, wakapiga kambi yao Iye-Abarimu, katika eneo la Moabu. Kutoka Iye-Abarimu, wakapiga kambi yao Diboni-Gadi. Kutoka Diboni-Gadi, wakasafiri na kupiga kambi yao Almoni-Diblataimu. Kutoka Almoni-Diblataimu, wakasafiri na kupiga kambi yao katika milima ya Abarimu, karibu na mulima Nebo. Kutoka milima ya Abarimu, wakasafiri na kupiga kambi yao katika mabonde ya Moabu ngambo ya muto Yordani karibu na Yeriko. Wakapiga kambi hiyo karibu na muto Yordani kati ya Beti-Yesimoti na bonde la Abeli-Sitimu kwenye mabonde ya Moabu. Katika mabonde ya Moabu, ngambo ya muto Yordani karibu na Yeriko, Yawe akamwambia Musa: Uwaambie Waisraeli kwamba mutakapovuka muto Yordani na kuingia katika inchi ya Kanana, muwafukuze wenyeji wote wa inchi hiyo mbele yenu. Mutaziharibu sanamu zao zote za mawe na za kuyeyushwa na kubomoa kila pahali pao pa ibada. Mutatwaa inchi hiyo na kukaa mule kwa sababu nimewapa muirizi. Mutagawanya inchi hiyo kwa kura kufuata jamaa zenu; eneo kubwa kwa kabila kubwa na eneo dogo kwa kabila dogo. Lakini kama musipowafukuza wenyeji wa inchi hiyo kwanza, basi wale mutakaowaacha watakuwa kama vile sindano ndani ya macho yenu au miiba kila upande, na watawasumbua. Nami nitawafanya ninyi kama vile nilivyokusudia kuwafanya wao. Yawe akamwambia Musa: Uwaamuru Waisraeli ukisema: Mutakapoingia Kanana, inchi ambayo ninawapa ikuwe inchi yenu, mipaka ya eneo lenu lote itakuwa kama hivi. Upande wa kusini mupaka wenu utakuwa kutoka jangwa la Sini kupitia upande wa Edomu. Utaanzia mashariki upande wa kusini mwisho wa bahari ya Chumvi. Kisha utapinda kusini kuelekea mupando wa Akarabimu na kupitia Sini mpaka Kadesi-Barnea, upande wa kusini. Kutoka pale, mupaka utapinda kuelekea kaskazini-magaribi mpaka Hasari-Adari na kupita mpaka Azimoni. Kutoka Azimoni utapinda kuelekea kijito cha Misri kwenye mupaka wa Misri na kuishia bahari ya Mediteranea. Mupaka wenu wa upande wa magaribi utakuwa bahari ya Mediteranea. Mupaka wenu wa upande wa kaskazini utakuwa kama hivi: kutoka bahari ya Mediteranea, mpaka kwenye mulima Hori, na kutoka mulima Hori, mpaka kwenye njia inayokwenda Hamati, na kuendelea mpaka Sedadi, kupitia Zifuroni na kuishia Hazari-Enani. Huo utakuwa mupaka wenu wa kaskazini. Mupaka wenu wa upande wa mashariki mutauweka kutoka Hazari-Enani mpaka Sefamu. Kutoka Sefamu utaelekea kusini mpaka Ribla, upande wa mashariki wa Aini; kisha mupaka huo utakwenda chini mpaka kwenye muteremuko wa upande wa mashariki wa ziwa la Kinereti, halafu utateremuka kufuata muto Yordani mpaka bahari ya Chumvi hii ndiyo itakuwa inchi yako kama vile mupaka unavyokuwa. Basi, Musa akawaambia Waisraeli: Hii ndiyo inchi mutakayoirizi kwa kupiga kura, inchi ambayo Yawe ameagiza ipewe kwa makabila tisa na nusu. Kabila la Rubeni na la Gadi, na nusu ya kabila la Manase yamepata urizi wao kulingana na ukoo zao. Makabila hayo mawili na nusu yamepata urizi wao ngambo ya muto Yordani upande wa mashariki, kuelekea Yeriko, jua linakotokea. Yawe akamwambia Musa: Kuhani Eleazari na Yoshua mwana wa Nuni ndio watakaowagawanyia watu inchi kuwa mali yao. Utatwaa vilevile kiongozi mumoja kutoka kila kabila kwa kusaidia katika ugawanyaji wa inchi. Haya ndiyo majina yao: Kabila la Yuda, Kalebu mwana wa Yefune. Kabila la Simeoni, Semweli mwana wa Amihudi. Kabila la Benjamina, Elidadi mwana wa Kisiloni. Kabila la Dani, Buki mwana wa Yogli. Kabila la Manase mwana wa Yosefu, Hanieli mwana wa Efodi. Kabila la Efuraimu mwana wa Yosefu, Kemueli mwana wa Sifutani. Kabila la Zebuluni, Elisafani mwana wa Parnaki. Kabila la Isakari, Paltieli mwana wa Azani. Kabila la Aseri, Ahihudi mwana wa Selomi Kabila la Nafutali, Pedaheli mwana wa Amihudi. Hawa ndio watu ambao Yawe aliwaamuru wawagawanyie watu Waisraeli inchi ya Kanana kuwa mali yao. Yawe akasema na Musa katika mabonde ya Moabu, ngambo ya muto Yordani karibu na Yeriko, akamwambia: Uwaamuru Waisraeli kwamba kutokana na urizi watakaopewa, wawape Walawi miji ya kukaa na sehemu za malisho kandokando ya miji hiyo. Miji hiyo itakuwa yao, nao watakaa mule na malisho yake yatakuwa kwa ajili ya ngombe na mifugo yao pamoja na nyama wao wengine. Malisho ya maeneo mutakayowapa Walawi kandokando ya miji yataenea kila upande umbali wa metre mia ine na makumi tano kutoka kwenye kuta za miji hiyo. Kwa hiyo, eneo hilo la malisho litakuwa la metre mia tisa muraba na litaenea kila upande wa muji, muji wenyewe ukiwa katikati. Eneo hilo litakuwa malisho yao kandokando ya miji yao. Mutawapa Walawi miji sita ya makimbilio ambapo mutu akimwua mwenzake bila kukusudia ataruhusiwa kukimbilia. Pamoja na hiyo, mutawapa miji mingine makumi ine na miwili. Jumla ya miji mutakayowapa Walawi itakuwa makumi ine na minane; mutawapa miji hiyo pamoja na sehemu za malisho yake. Hesabu ya miji mutakayowapa Walawi katika urizi wa Waisraeli itategemea ukubwa wa kabila; kabila kubwa litatoa miji mingi na kabila dogo litatoa michache. Kila kabila litatoa miji yake kwa ajili ya Walawi kulingana na eneo litakalorizi. Yawe akaongea na Musa, akamwambia: Uwaambie Waisraeli kwamba wakati mutakapovuka muto Yordani na kuingia katika inchi ya Kanana, mutachagua miji itakayokuwa miji ya makimbilio ambamo kama mutu akimwua mwenzake bila kukusudia ataweza kukimbilia. Miji hiyo itakuwa pahali pa kukimbilia usalama kusudi huyo mwuaji asiuawe na mwenye kulipiza kisasi mbele ya kuhukumiwa na baraza la Waisraeli. Mutajitengea miji sita kwa ajili ya makimbilio. Kati ya miji hiyo sita mutakayotenga, mitatu ikuwe upande wa mashariki wa Yordani, na mitatu ikuwe katika inchi ya Kanana. Miji hii itakuwa ya makimbilio kwa ajili ya Waisraeli na wageni wa kudumu au wa muda wanaokaa pamoja nao. Mutu yeyote akimwua mwingine bila kukusudia anaweza kukimbilia huko. Lakini mutu akimupiga mwenzake kwa kitu cha chuma, na kumwua, mutu huyo ni mwuaji na anapaswa kuuawa. Mutu yeyote akimupiga mwenzake kwa jiwe, akikufa, mutu huyo ni mwuaji, anapaswa kuuawa. Kama akimupiga mwenzake kwa silaha ya muti ambayo inaweza kusababisha kifo, akikufa, mutu huyo ni mwuaji, na anapaswa kuuawa. Ndugu wa karibu wa mutu aliyeuawa atalipiza kisasi. Huyu atakapokutana na huyo mwuaji, atatimiza hukumu ya kifo. Vilevile, kama mutu anamuchukia mwenzake halafu, akimusukuma au kumutupia kitu kwa kumuvizia, au kwa kumupiga ngumi akikufa, basi mutu huyo aliyemupiga mwenzake ni mwuaji na anapaswa kuuawa. Ndugu wa karibu wa mutu aliyeuawa atalipiza kisasi atakapokutana naye. Lakini kama mutu akimusukuma mwenzake kwa rafla bila chuki au kumutupia kitu bila kumuvizia au mutu akirusha jiwe linaloweza kusababisha kifo, na kuua mutu bila kukusudia, ingawa hakukukuwa madeni kati yao na huyo aliyeua hakukusudia kumuzuru, basi, baraza lile litaamua kati ya huyo mwuaji na jamaa ya mutu aliyeuawa anayetaka kulipiza kisasi, kulingana na maagizo haya. Baraza litamwokoa mutu huyo aliyeua toka katika mikono ya ndugu ya mutu aliyeuawa, na kumurudisha katika muji wa makimbilio alimokuwa amekimbilia. Atakaa huko mpaka kufa kwa Kuhani Mukubwa wa wakati ule aliyechaguliwa kwa kupakwa mafuta matakatifu. Lakini huyo aliyeua akitoka inje ya muji aliokimbilia wakati wowote, halafu ndugu ya mutu aliyeuawa akimukuta inje ya mipaka ya muji huo wa makimbilio akimwua, huyo hatakuwa na kosa la kuua. Maana huyo aliyeua anapaswa kukaa ndani ya muji wa makimbilio mpaka Kuhani Mukubwa atakapokufa; lakini kisha kufa kwa Kuhani Mukubwa anaweza kurudi kwake. Sheria hizi zitakuwa masharti na maagizo katika vizazi vyenu vyote, pahali popote mutakapokaa. Mutu yeyote atakayeua mutu, atahukumiwa kifo kutokana na ushuhuda wa washuhuda wawili au zaidi; mutu yeyote hawezi kuhukumiwa kifo kutokana na ushuhuda wa mutu mumoja. Musipokee malipo yoyote kwa kuokoa maisha ya mwuaji aliyepatikana na kosa, akihukumiwa kifo; mutu huyo anapaswa kuuawa. Musipokee wala musikubali malipo yoyote kutoka kwa mutu aliyekimbilia katika muji wa makimbilio kwa kumuruhusu arudi kukaa kwake mbele ya kifo cha Kuhani Mukubwa. Mukifanya hivyo mutachafua inchi ambayo munakaa ndani yake. Umwangaji wa damu unachafua inchi, na hakuna sadaka inayoweza kutakasa inchi iliyofanyiwa mauaji isipokuwa kwa kumwua mwuaji huyo. Musichafue inchi ambayo munakaa ndani yake, inchi ambayo mimi ninakaa ndani yake; maana mimi Yawe ninakaa kati yenu Waisraeli. Viongozi wa jamaa katika ukoo wa Gileadi mwana wa Makiri, mwana wa Manase mwana wa Yosefu, wakakwenda kuzungumuza na Musa na viongozi wengine wa ukoo za Waisraeli. Wakasema: Yawe alikuamuru kuwagawanyia watu wa Israeli inchi kwa kura kuwa urizi wao; alikuamuru vilevile uwape wabinti za Selofehadi ndugu yetu urizi wa baba yao. Lakini wao wakiolewa na Waisraeli wa makabila mengine, urizi wao utatoka kwetu na kuwaendea watu wa kabila watakamoolewa; kwa hiyo urizi wetu sisi utapunguka. Katika sikukuu ya ukumbusho urizi wao utahesabiwa pamoja na ule wa kabila watakamoolewa na hivyo kabila letu halitapata urizi huo tena. Basi, Musa akawapa Waisraeli agizo lile kutoka kwa Yawe, akawaambia: Watu wa ukoo wa kabila la Yosefu wamesema ukweli. Na hivi ndivyo Yawe anavyoamuru juu ya wabinti za Selofehadi; wako huru kuolewa na mutu yeyote wanayemupenda, lakini waolewe katika kabila lao, kusudi urizi wa Waisraeli usihamishiwe kwa kabila lingine; kila Mwisraeli atabakia na urizi wa kabila lake. Mwanamuke yeyote mwenye urizi katika kabila moja la Israeli anapaswa kuolewa na mutu wa kabila lake, kusudi kila Mwisraeli abakie na urizi wa babu zake. Hivyo hakutakuwa urizi wowote utakaohamishwa kutoka kabila moja kwa lingine. Kila kabila la Waisraeli litashikilia urizi wake. Wabinti za Selofehadi wakafanya kama vile Yawe alivyomwamuru Musa. Wote: Mala, Tirsa, Hogla, Milka na Noa wakaolewa na binamu zao. Wakaolewa katika jamaa za ukoo wa Manase mwana wa Yosefu, na urizi wao ukabaki katika kabila la baba yao. Hizo ndizo amri na maagizo ambayo Yawe aliwapa Waisraeli kwa njia ya Musa katika mabonde ya Moabu, ngambo ya muto Yordani karibu na muji wa Yeriko. Kitabu hiki kina maneno ambayo Musa aliwaambia watu wote wa Israeli wakati walipokuwa katika jangwa upande wa mashariki wa muto Yordani. Walikuwa katika bonde la Yordani karibu na Sufu, kati ya muji wa Parani upande mumoja na miji ya Tofeli, Labani, Hazeroti na Dizahabu upande mwingine. (Ni mwendo wa siku kumi na moja kutoka mulima Horebu mpaka Kadesi-Barnea kwa njia ya mulima Seiri.) Siku ya kwanza ya mwezi wa kumi na moja, mwaka wa makumi ine nyuma ya kutoka Misri, Musa akawaambia watu kila kitu ambacho Yawe alimwamuru awaambie. Alifanya hivyo kisha Yawe kumushinda mufalme Sihoni wa Waamori ambaye alikuwa anakaa katika muji wa Hesiboni, na mufalme Ogi wa Basani ambaye alikuwa anakaa katika muji wa Astaroti na Edirei. Musa akaanza kuwaelezea watu sheria ya Mungu wakati walipokuwa upande wa mashariki wa muto Yordani. Akawaambia hivi: “Tulipokuwa kwenye mulima Sinai, Yawe, Mungu wetu, alituambia hivi: ‘Mumekaa muda wa kutosha kwenye mulima huu. Sasa muvunje kambi yenu muendelee na safari. Muende kwenye inchi ya milima ya Waamori na maeneo ya inchi jirani katika Araba, kwenye milima na mabonde, huko Negebu na sehemu za pembeni ya bahari. Muende mpaka inchi ya Kanana, na inchi ya Lebanoni, mpaka kwenye ule muto mukubwa Furati. Inchi hii yote nimeiweka mbele yenu. Basi, muende kutwaa inchi hiyo ambayo mimi Yawe niliapa kuwapa wazee wenu Abrahamu, Isaka, Yakobo na wazao wao.’ ” Musa akawaambia watu: “Tulipokuwa tungali kwenye mulima Sinai, mimi niliwaambia hivi: ‘Siwezi mimi mwenyewe kubeba muzigo wa kuwaongoza ninyi peke yangu. Yawe, Mungu wenu, amewafanya mukuwe wengi; leo mumekuwa wengi kama vile nyota za mbinguni. Yawe, Mungu wa babu zenu, awafanye muzidi kuongezeka mara elfu zaidi ya vile munavyokuwa sasa na kuwabariki kama vile alivyoahidi! Lakini mimi peke yangu nitaweza namna gani kubeba muzigo wa kuamua matatizo yenu, mashitaki yenu na magomvi yenu? Muchague kutoka katika kila kabila watu wenye hekima, akili na ujuzi kusudi niwafanye wakuwe viongozi wenu.’ Ninyi mulikubali, mukanijibu hivi: ‘Jambo ulilosema ni jema kwetu kufanya’. Hivyo nikatwaa wale viongozi wenye hekima, akili na ujuzi ambao muliwachagua kutoka katika makabila yenu, nikawaweka kuwa viongozi wenu. Nikawaweka wengine kuwa majemadari wa makundi ya watu elfu moja moja, ya watu mia moja moja, ya watu makumi tano tano na ya watu kumi kumi. Nikachagua vilevile wakubwa wengine wa kuchunga kila kabila. “Wakati uleule nikawapa waamuzi wenu maagizo haya: ‘Musikilize maneno ya watu wenu. Mutoe hukumu za haki katika maneno kati ya kila mumoja na ndugu yake au na wageni wanaoishi pamoja nanyi. Musipendelee mutu yeyote katika kutoa hukumu; mutawasikiliza bila upendeleo, wakubwa kwa wadogo. Musiogopeshwe na sura ya mutu, maana ninyi mutapaswa kuhukumu kwa ajili ya Mungu. Kukikuwa maneno ambayo ni magumu sana kwenu, mutayafikisha kwangu nami nitayasikiliza.’ Wakati huohuo, nikawaagiza mambo yote munayopaswa kufanya. “Basi, kama vile Yawe, Mungu wetu, alivyotuamuru, tukaanza safari yetu kutoka mulima Horebu, tukapita katika lile jangwa kubwa la kutisha munalojua, kwa kufuata njia inayoelekea inchi ya milima ya Waamori. Tulipofika Kadesi-Barnea, mimi nikawaambia: ‘Sasa mumefika katika inchi ya milima ya Waamori ambayo Yawe, Mungu wetu, ametupatia. Muangalie, Yawe, Mungu wenu, ameiweka inchi hii mbele yenu. Basi! Muende, muirizi kama vile Yawe, Mungu wa wazee wenu alivyowaambia. Musiogope wala musifazaike!’ “Kisha wote mukakuja karibu nami mukaniambia: ‘Tutume watu watutangulie, wapeleleze inchi, halafu warudi kutujulisha njia bora ya kufuata na miji gani tutakuta huko.’ Jambo hilo likaonekana kuwa zuri kwangu, nikawachagua watu kumi na wawili, mutu mumoja kutoka katika kila kabila. Watu hao wakakwenda katika inchi ile ya milima, wakafika kwenye bonde la Eskoli na kulipeleleza. Waliporudi, wakatuletea matunda mamoja ya inchi hiyo na wakatuarifu kwamba inchi hiyo Yawe, Mungu wetu, anayotupatia ni nzuri. “Lakini ninyi hamukufuata agizo la Yawe, Mungu wenu; mulikataa kwenda katika inchi hiyo. Mulinungunika ndani ya mahema yenu mukisema: ‘Yawe anatuchukia na ndiyo maana alitutoa katika inchi ya Misri. Alitaka kututia katika mikono ya Waamori kusudi atuangamize. Kwa nini tuende huko wakati tumevunjika moyo kwa hofu? Wametuambia kwamba watu wa huko ni wakubwa na warefu kuliko sisi, na kwamba miji yao ni mikubwa na yenye kuta zinazofika katika mawingu. Tena wamesema kwamba waliwaona wale wazao wa Anaki!’ “Lakini mimi nikawaambia hivi: ‘Musikuwe na hofu wala musiwaogope watu hao.’ Yawe, Mungu wenu, ambaye anawatangulia, yeye mwenyewe atapigana kwa ajili yenu kama vile alivyofanya mbele yenu kule Misri na kule katika jangwa ambako muliona jinsi alivyowabeba safari hiyo yote kama vile baba anavyobeba mwana wake, mpaka mukafika hapa. Lakini ingawa nilisema hayo yote, ninyi hamukumwamini Yawe, Mungu wenu, ambaye aliwatangulia katika njia na kuwatafutia pahali pa kupiga kambi zenu. Usiku aliwatangulia kwa moto na muchana kwa wingu, kwa kuwaonyesha njia. “Yawe akasikia manunguniko yenu, akakasirika, akaapa akisema: ‘Hakuna hata mumoja wenu katika kizazi hiki kiovu atakayeingia katika ile inchi nzuri niliyoahidi kuwapa wazee wenu. Kalebu mwana wa Yefune, ndiye tu atakayeiona. Nami nitamupatia inchi hiyo aliyokanyaga ndani ikuwe yake yeye na wazao wake kwa sababu amekuwa mwaminifu kabisa kwangu.’ Yawe akanikasirikia mimi vilevile kwa sababu yenu, akasema: ‘Hata wewe Musa hautaingia katika inchi hiyo. Lakini musaidizi wako Yoshua mwana wa Nuni ataingia humo. Basi, umutie moyo maana yeye atawaongoza watu wa Israeli wairizi inchi hiyo’. Kisha Yawe akatuambia sisi wote: ‘Hao watoto wenu munaoogopa kwamba watakuwa mateka za waadui zenu, hakika hao wanaokuwa wadogo ambao hawajui bado kupambanua kati ya mazuri na mabaya, hao ndio watakaoingia huko, nami nitawapa wao inchi hiyo ikuwe yao. Lakini ninyi, mugeuke na kurudi katika jangwa kuelekea bahari Nyekundu.’ “Kisha mukanijibu: ‘Sisi tumemutendea Yawe zambi, lakini sasa tutakwenda na kupigana kama vile Yawe, Mungu wetu alivyotuamuru’. Hivyo, kila mumoja wenu akajitayarisha kupigana vita, maana mulifikiri kwamba lingekuwa jambo jepesi kuishambulia inchi hiyo ya milima. Naye Yawe akaniambia: ‘Uwaambie hao watu wasiende kupigana kwa sababu siko pamoja nao. Wasiende, kusudi wasishindwe na waadui zao’. Basi, mimi nikawaambia hivyo, lakini ninyi hamukusikia. Pahali pake mukakataa kufuata agizo la Yawe. Bila kujali mukaingia katika inchi hiyo ya milima. Hapo, Waamori waliokuwa wanaishi katika eneo hilo la milima wakateremuka kuwashambulia na kama vile nyuki wanavyofanya wakawapiga huko Seiri mpaka Horma. Ndipo muliporudi, mukamulilia Yawe, lakini hakuwasikiliza wala hakuwajali. Basi, mukabaki kule Kadesi kwa muda murefu ambao mulikaa kule. “Kisha, tukageuka, tukasafiri katika jangwa kwa kupitia njia ya bahari Nyekundu, kama vile Yawe alivyoniambia. Tukatangatanga karibu na mulima Seiri kwa muda murefu. Kisha Yawe akaniambia: ‘Mumetangatanga ya kutosha katika inchi hii ya milima. Sasa mugeuke muelekee upande wa kaskazini. Muko karibu kupita katika inchi ya milima ya Seiri, inchi ya wandugu zenu wazao wa Esau. Hao watawaogopa, lakini mufanye angalisho, musipigane nao kwa sababu sitawapa sehemu yoyote ya inchi yao. Sitawapa hata pahali padogo pa kukanyaga. Inchi hiyo ya milima ya Seiri nimewapa wazao wa Esau ikuwe mali yao. Mukitaka chakula au maji kutoka kwao, munapaswa kununua.’ “Basi, mukumbuke jinsi Yawe Mungu wenu alivyowabariki ninyi katika kila jambo mulilofanya. Aliwatunza mulipokuwa munatangatanga katika jangwa hili kubwa. Amekuwa pamoja nanyi miaka hii yote makumi ine na hamukupungukiwa na kitu chochote. “Hivyo tukaendelea na safari yetu, tukawapita wandugu zetu, wazao wa Esau ambao waliishi Seiri, tukaepuka vilevile ile njia ya bonde na sehemu za miji ya Elati na Esioni-Geberi. Kisha tukageuka tukafuata njia ya kupitia jangwa la Moabu. Yawe akaniambia: ‘Usiwasumbue watu wa Moabu, wala usipigane nao maana sitawapa sehemu yoyote ya inchi yao. Lakini eneo hilo la Ari nimewapa hao wazao wa Loti likuwe mali yao.’ (Hapo zamani hiyo inchi ya Ari ilikuwa imekaliwa na watu wengi, wenye nguvu na ambao walikuwa warefu kama vile Waanaki. Kama vile Waanaki, watu hawa walijulikana vilevile kama Warefai, lakini Wamoabu waliwaita Waemi. Wahori vilevile waliishi huko Seiri zamani, lakini wazao wa Esau wakawafukuza na kuwaangamiza, kisha wao wenyewe wakakaa katika eneo hilo pahali pao. Waisraeli wakafanya vile vile katika inchi ile ambayo Yawe aliwapa ikuwe mali yao.) “Yawe akatuambia: ‘Muondoke sasa, muvuke kijito Zeredi’. Basi, tukavuka kijito Zeredi. Miaka makumi tatu na nane ilikuwa imepita tangu kuondoka Kadesi-Barnea mpaka kuvuka kijito Zeredi. Wakati huo, wote wenye umri wa kwenda kwa vita waliotoka Misri walikuwa wamekwisha kufa, kulingana na jinsi Yawe alivyowaapia. Yawe mwenyewe akawashambulia watu hao kwa kuwaangamiza huko katika kambi, hata wote wakaisha. “Basi, watu hao wote walipokwisha kufa, Yawe akaniambia: ‘Leo hii mutauvuka mupaka wa Moabu kwa kupitia inchi ya Ari. Mutaifikia inchi ya Waamoni. Musiwasumbue wala musipigane nao kwa sababu sitawapa sehemu yoyote ya hao wazao wa Amoni ikuwe mali yenu. Hao ni wazao wa Loti, na nimewapa hiyo inchi ikuwe mali yao.’ ” (Inchi hiyo inajulikana vilevile kama inchi ya Warefai. Warefai walikuwa wanaishi huko hapo zamani; Waamoni waliwaita hao Wazamuzumi. Walikuwa watu wengi, wenye nguvu na warefu kama vile Waanaki. Lakini Yawe akawaangamiza mbele ya Waamori ambao walitwaa inchi yao wakaishi humo pahali pao. Yawe akafanya kama vile alivyowafanyia wazao wa Esau ndio Waedomu, ambao wanaishi katika inchi ya Seiri. Aliwaangamiza Wahori wakati Waedomu walipofika huko, wakanyanganya inchi yao na kuishi humo mpaka leo. Waavi walikuwa zamani wakiishi katika vijiji vya kando ya Mediteranea mpaka Gaza. Wakafutori kutoka kisiwa cha Kafutori wakawaangamiza, wakaishi humo pahali pao.) “Kisha Yawe akatuamuru: ‘Basi! Muanze safari. Muvuke bonde la Arnoni. Mimi nimetia katika mikono yenu Sihoni, mufalme wa Waamori wa Hesiboni na inchi yake. Mushambulie na kuanza kurizi inchi yake. Leo nitaanza kuwafanya watu wote katika dunia wakuwe na woga na hofu juu yenu. Watasikia habari zenu nao watatetemeka na kufazaika.’ “Basi, nikatuma watu kutoka jangwa la Kedemoti waende kwa mufalme Sihoni wa Hesiboni na ujumbe huu wa amani: ‘Uturuhusu tupite katika inchi yako. Tutapitia katika barabara na kwenda moja kwa moja bila kugeuka kuume wala kushoto. Chakula chetu tutakinunua kwako na maji ya kunywa vilevile. Tunachoomba tu ni ruhusa ya kupita kwa miguu katika inchi yako, tuvuke muto Yordani na kuingia katika inchi ambayo Yawe, Mungu wetu anatupatia. Wazao wa Esau wanaoishi Seiri na Wamoabu wanaoishi Ari walituruhusu vilevile kupita katika inchi yao’. “Lakini Sihoni, mufalme wa Hesiboni, hakuturuhusu tupite katika inchi yake. Yawe, Mungu wenu, akamufanya akuwe na kichwa kigumu na mugumu wa moyo, kusudi tumushinde na kutwaa inchi yake ambayo tunairizi mpaka leo. “Halafu Yawe akaniambia: ‘Nimeanza kumutia mufalme Sihoni na inchi yake katika mikono yenu. Muanze kutwaa inchi yake na kuirizi’. Kisha Sihoni akatoka na watu wake wote kupigana nasi karibu na muji wa Yahasa. Naye Yawe, Mungu wetu, akamutoa, tukamushinda yeye, watoto wake na watu wake wote. Tukaiteka na kuiharibu miji yake yote, tukaua wanaume na wanawake na watoto. Hatukumwacha mutu yeyote muzima. Tulibeba tu mifugo na mali tuliyokuta katika miji tuli Yosinda. Kuanzia Aroeri, muji unaokuwa kwenye ukingo wa bonde la Arnoni, na ule muji mwingine unaokuwa ndani ya bonde hili mpaka inchi ya Gileadi, hakuna muji wowote ambao hatukuweza kuushinda. Yawe aliitia miji yote katika mikono yetu. Lakini hatukukaribia inchi ya Waamoni au ukingo wa muto Yaboki wala katika miji ya inchi ya milima wala sehemu yoyote ambayo Yawe, Mungu wetu, alitukataza. “Kisha, tukageuka, tukapanda kuelekea Basani. Mufalme Ogi akatoka na watu wake wote kwa kupigana nasi karibu na muji wa Edirei. Lakini Yawe akaniambia: ‘Usimwogope, maana nimemutia katika mikono yako pamoja na watu wake na inchi yake. Utamutendea kama vile ulivyomutendea Sihoni mufalme wa Waamori aliyekaa kule Hesiboni’. “Basi, Yawe akamutia katika mikono yetu mufalme Ogi wa Basani na watu wake, tukawaangamiza hata hakukubakia mutu yeyote. Tukateka miji yake yote; hakuna hata muji mumoja ambao hatukuuteka. Kwa jumla tuliteka miji makumi sita, ni kusema eneo lote la Argobu ambalo lilitawaliwa na mufalme Ogi wa Basani. Miji yote hii ilikuwa na makimbilio yenye kuta ndefu zilizokuwa na milango na vifungio. Kulikuwa vilevile vijiji vingi ambavyo havikuzungukwa na kuta. Tuliteketeza kila kitu huko, tukaharibu kila muji na kuua wanaume, wanawake na watoto kama vile tulivyofanya katika miji ya mufalme Sihoni wa Hesiboni. Lakini mifugo yote na mali tukaviteka. “Wakati huo tukatwaa inchi hiyo ya wale wafalme wawili wa Waamori waliokuwa wanakaa ngambo ya muto Yordani, katikati ya muto Arnoni na mulima Hermoni. (Wasidoni wanaita mulima huo Sirioni, nao Waamori wanauita Seniri.) Tukateka miji yote katika sehemu za mabonde, za mwinuko, na vilevile eneo lote la Gileadi na Basani mpaka Saleka na Edirei, miji ya mufalme Ogi huko Basani.” (Mufalme Ogi ndiye peke yake aliyebakia kati ya Warefai. Kitanda chake kilichotengenezwa kwa chuma, kilikuwa na urefu wa metre ine na upana wa karibu metre mbili. Kitanda hicho kipo katika muji wa Waamori wa Raba.) “Tulipoitwaa inchi hiyo, nikawapa makabila ya Rubeni na Gadi eneo la kuanzia upande wa kaskazini wa Aroeri karibu na Arnoni na nusu ya eneo la milima ya Gileadi, pamoja na miji yake. Kisha nikalipatia nusu ya lile kabila la Manase sehemu iliyobaki ya Gileadi pamoja na Basani yote iliyotawaliwa na Ogi, ni kusema eneo lote la Argobu. Inchi yote ya Basani ilijulikana kama vile inchi ya Warefai. Yairi, mutu wa kabila la Manase, alitwaa eneo lote la inchi ya Argobu, ni kusema Basani, mpaka kwenye mupaka wa Gesuri na Maka. Vijiji vyote alivipa jina lake, na mpaka leo vinajulikana kama vile ‘Vijiji vya Yairi’. Watu wa ukoo wa Makiri wa kabila la Manase nikawapa Gileadi, na watu wa makabila ya Rubeni na Gadi nikawapa inchi yote kutoka Gileadi mpaka muto Arnoni. Mupaka wao wa kusini ulikuwa muto ule na wa kaskazini ulikuwa muto Yaboki ambao ndio unaopakana na inchi ya Waamori. Upande wa magaribi, inchi yao ilienea mpaka muto Yordani. Toka ziwa Galilaya upande wa kaskazini, ukashuka mpaka kwenye bahari ya Araba, ni kusema bahari ya Chumvi, mpaka kwenye miteremuko ya Pisiga, upande wa mashariki. “Wakati ule niliwapa maagizo haya: ‘Yawe, Mungu wenu amewapa inchi hii upande wa mashariki wa muto Yordani ikuwe mali yenu. Sasa ninyi mashujaa kati ya wandugu zenu, mutwae silaha muvuke muto Yordani mukiwa mbele ya wandugu zenu Waisraeli. Lakini wake zenu, watoto wenu na nyama wenu – ninajua muko na mifugo mingi – watabaki kwenye miji niliyowapa. Muwasaidie wandugu zenu Waisraeli mpaka Yawe atakapowajalia watulie pahali pao kama vile nanyi mulivyotulia, ni kusema nao vilevile warizi inchi ambayo Yawe, Mungu wenu, anawapatia huko ngambo ya Yordani. Nyuma ya hayo, mutaweza kurudia katika inchi yenu hii ambayo nimewapa ikuwe yenu!’ “Kisha nikamwamuru Yoshua: ‘Wewe umeona kwa macho yako mambo yote ambayo Yawe, Mungu wako, amewatendea wafalme hawa wawili, Sihoni na Ogi. Basi, yeye atawatendea vile vile wafalme wa inchi zote mutakazopitia. Musiwaogope maana Yawe, Mungu wenu, ndiye atakayepigana kwa ajili yenu.’ “Wakati huo nikamusihi Yawe nikisema: ‘Ee Bwana wetu Yawe, ninajua umenionyesha mimi mutumishi wako mwanzo tu wa ukubwa wako na uwezo wako. Maana, kuna mungu gani huko mbinguni au katika dunia anayeweza kufanya mambo makubwa na ya ajabu kama vile ulivyofanya wewe? Ninakuomba nivuke muto Yordani, niione inchi hiyo nzuri upande wa magaribi wa Yordani, hakika, inchi nzuri ya kupendeza ya milima, pamoja na milima ya Lebanoni’. “Lakini Yawe akanikasirikia kwa sababu yenu, akakataa kunisikiliza. Pahali pake akaniambia: ‘Inatosha! Usiseme tena jambo hili. Panda mpaka kwenye kilele cha mulima Pisiga, uangalie vizuri upande wa magaribi, kaskazini, kusini na mashariki, na kuiona inchi hiyo; lakini wewe hautavuka huu muto Yordani. Lakini umupe Yoshua maagizo, umutie moyo na kumwimarisha, maana yeye ndiye atakayewaongoza watu hawa mpaka ngambo, kurizi inchi utakayoiona’. “Basi, tukabaki hapa katika bonde mbele ya Beti-Peori.” Musa akaendelea kusema: “Mushike basi na kufuata masharti na maagizo niliyowafundisha, kusudi mupate kuishi na kurizi inchi ambayo Yawe, Mungu wa babu zenu, anawapa. Musiongeze chochote katika amri ninazowapa, wala musipunguze kitu. Mushike amri za Yawe, Mungu wenu, ambazo ninawapa. Ninyi muliona kwa macho yenu mambo ambayo Yawe aliyafanya juu ya Bali-Peori. Yawe, Mungu wenu, aliwaangamiza watu wote kati yenu waliomwabudu huyo mungu Bali-Peori. Lakini ninyi muliokuwa waaminifu kwa Yawe, Mungu wenu muko wazima mpaka leo. “Muangalie! Nimewafundisha masharti na maagizo kama vile Yawe, Mungu wangu alivyoniamuru nifanye, kusudi muyashike katika inchi munayokwenda kuirizi. Mushike na kutimiza masharti na maagizo hayo maana mukifanya hivyo watu wa mataifa mengine watakapopata kujua masharti hayo, watatambua kwamba ninyi ni wenye hekima na akili. Watasema hivi: ‘Kweli watu wa taifa hili kubwa wana hekima na akili!’ “Hakuna taifa lolote hata likuwe kubwa namna gani, ambalo mungu wake yuko karibu nalo, kama vile Yawe, Mungu wetu, anavyokuwa karibu nasi tunapomwomba musaada. Wala hakuna taifa lingine lolote hata likuwe kubwa namna gani, lenye masharti na maagizo ya haki, kama hayo ambayo nimewafundisha siku hii ya leo. “Lakini mukuwe waangalifu na kufanya angalisho sana kusudi musisahau mambo yale muliyoona kwa macho yenu wenyewe, kusudi isitokee hata mara moja katika maisha yenu mambo hayo kusahaulika ndani ya mioyo yenu. Muwaelezee watoto wenu na wajukuu wenu juu ya siku ile ambayo mulisimama mbele ya Yawe, Mungu wenu, kule Horebu, ndio Sinai, aliponiambia: ‘Muwakusanye hao watu mbele yangu, niwaambie maneno yangu kusudi wajifunze kuniogopa mimi siku zote za maisha yao, na kuwafundisha watoto wao kufanya hivyo’. “Basi, mulikaribia na kusimama chini ya ule mulima ambao wakati huo ulikuwa unawaka moto uliofika mpaka mbinguni ukiwa umetanda giza na wingu zito. Kisha Yawe akasema nanyi kutoka katikati ya moto huo. Mukasikia maneno aliyosema lakini hamukumwona. Mulisikia tu sauti yake. Naye akawatangazia agano lake akawaamuru mulishike maana yake mutii zile amri kumi ambazo aliandika juu ya vibao viwili vya mawe. Wakati huo Yawe akaniamuru niwafundishe masharti na maagizo yote ambayo munapaswa kutimiza katika inchi munayokwenda kuirizi. “Kwa hiyo mukuwe waangalifu kusudi musisahau kwamba Yawe aliposema nanyi kule kwenye milima ya Horebu katikati ya moto hamukumwona kwa umbo. Kwa sababu hiyo mufanye angalisho sana, musipotoke kwa kujifanyia sanamu yoyote ya kuchonga, au ya umbo au mufano wowote, mufano wa wanaume au wanawake, wa nyama yeyote katika dunia au ndege, au mufano wa nyama anayetambaa juu ya udongo au wa samaki ndani ya maji. Mufanye angalisho kusudi wakati mutakapoangalia na kuona nyota, vitu vyote vya mbinguni, musivutwe kuviabudu na kuvitumikia. Vitu hivyo Yawe amewaachia watu wengine waviabudu. Lakini ninyi ndio watu aliowakomboa kutoka Misri katika furu la chuma. Aliwatoa huko kusudi mukuwe watu wake kama vile munavyokuwa hivi leo. Kwa sababu yenu Yawe, Mungu wenu, alinikasirikia, akaapa kwamba mimi sitavuka muto Yordani kuingia katika inchi ile nzuri anayowapa ikuwe mali yenu. Mimi nitakufia katika inchi hii wala sitauvuka muto, lakini ninyi muko karibu kuuvuka na kwenda kurizi inchi ile nzuri. Mufanye angalisho sana kusudi musisahau agano ambalo Yawe, Mungu wenu, amefanya nanyi. Musijifanyie sanamu ya kuchonga katika umbo la kitu chochote ambacho Yawe, Mungu wenu, amewakataza kumufananisha nacho, maana Yawe, Mungu wenu, ni moto unaoteketeza. Yeye ni Mungu mwenye wivu. Yawe atawatawanya kati ya mataifa mengine, na ni wachache tu wenu watakaobakia huko ambako Yawe atawafukuzia. Huko mutatumikia miungu ya miti na mawe ambayo imetengenezwa kwa mikono ya watu na ambayo haiwezi kuona, haisikii, haikuli wala kunusa. Kisha kutoka humohumo katika inchi mutamutafuta Yawe, Mungu wenu, nanyi mutamupata kama mukimutafuta kwa moyo wote na roho yote. Mambo haya yote yatakapowapata huko, kisha mukipata taabu, mutamurudilia Yawe na kumutii. Yawe, Mungu wenu, ni Mungu mwenye rehema, hatawaachilia wala kuwaangamiza, wala kusahau agano ambalo alifanya na wazee wenu kwa kiapo. “Mufikiri sana juu ya matukio ya zamani, mambo yaliyotukia mbele ninyi hamujazaliwa, tangu siku ile Mungu alipomwumba mutu katika dunia. Muulize katika ulimwengu wote, toka pembe moja mpaka nyingine, kama jambo la ajabu la namna hii limepata kutokea au kusikilika! Watu walikwisha kusikia sauti ya Mungu ikisema toka katikati ya moto, kama ninyi mulivyosikia, wakabaki wazima? Kuna Mungu yeyote mwingine aliyejaribu hata kidogo kwenda kujitwalia taifa lake kutoka taifa lingine, kama vile Yawe, Mungu wenu, alivyofanya, kwa kutumia majaribio, vitambulisho, maajabu, vita, na vitisho? Hapana. Lakini mulishuhudia kwa macho yenu namna Yawe alivyofanya kwa mukono wake wenye nguvu kabisa kule Misri. Ninyi mulijaliwa kuona mambo hayo, kusudi mupate kutambua kwamba Yawe ndiye peke yake Mungu na wala hakuna mwingine. Aliwafanya muisikie sauti yake kutoka mbinguni kusudi aweze kuwafundisha; na hapa katika dunia akawafanya muone moto wake mukubwa na kusikia maneno yake kutoka katikati ya moto huo. Kwa kuwa aliwapenda wazee wenu, yeye amewachagua ninyi wazao wao, akawatoa yeye mwenyewe katika inchi ya Misri kwa nguvu yake kubwa. Alifukuza mbele yenu mataifa makubwa na yenye nguvu kuliko ninyi, kusudi awalete na kuwapa inchi yao ikuwe urizi wenu, kama vile inavyokuwa mpaka leo! Basi, mukumbuke leo na kuweka ndani ya mioyo yenu, kwamba Yawe ndiye Mungu juu mbinguni na chini katika dunia. Hakuna mwingine. Kwa hiyo mushike masharti yake na amri zake ambazo ninawapa leo kusudi mufanikiwe, ninyi pamoja na wazao wenu, na kuishi siku nyingi katika inchi ambayo Yawe, Mungu wenu, anawapa ikuwe yenu milele.” Halafu Musa akatenga miji mitatu upande wa mashariki ya muto Yordani, ambamo mutu ataweza kukimbilia na kujiponyesha, kama ameua mutu ambaye si adui yake kwa bahati mbaya. Mutu kama huyo ataweza kukimbilia katika muji mumoja na kuyaokoa maisha yake. Alitenga muji wa Beseri katika bonde la jangwa kwa ajili ya kabila la Rubeni, muji wa Ramoti katika inchi ya Gileadi kwa ajili ya kabila la Gadi, na muji wa Golani katika inchi ya Basani kwa ajili ya kabila la Manase. Hii ndiyo sheria ambayo Musa aliwapa Waisraeli. Haya ndiyo maagizo, masharti na maamuzi ambayo Musa aliwaambia Waisraeli walipotoka Misri, wakiwa ngambo ya muto Yordani, katika bonde linalokuwa mbele ya Beti-Peori, katika inchi iliyokuwa ya mufalme Sihoni wa Waamori, aliyetawala kutoka katika muji wa Hesiboni, ambaye Musa na Waisraeli walimushinda walipotoka Misri. Walitwaa inchi yake na inchi ya mufalme Ogi wa Basani. Wafalme hao wawili wa Waamori walitawala huko upande wa mashariki wa muto Yordani. Inchi hiyo ilienea toka Aroeri kwenye ukingo wa muto Arnoni, mpaka mulima Sirioni, ni kusema Hermoni, pamoja na eneo lote upande wa mashariki wa muto Yordani mpaka bahari ya Chumvi, kwa mwisho wa miteremuko ya mulima Pisiga. Musa akawaita pamoja Waisraeli, akawaambia: “Enyi Waisraeli, musikilize masharti na maagizo ambayo ninayasema mbele yenu leo. Mujifunze hayo na kuyatimiza kwa uangalifu. Yawe, Mungu wetu, alifanya agano nasi kwenye mulima Horebu. Hakufanya agano hilo na wazee wetu, lakini alilifanya na sisi wote ambao tuko wazima hivi leo. Yawe alisema nanyi kinywa kwa kinywa huko kwenye mulima katikati ya moto. Wakati huo mimi nikasimama kati yenu na Yawe, nikawatangazia yale aliyosema, kwa sababu ninyi muliogopa ule moto na hamukupanda juu ya mulima. Yawe akasema hivi: “Mimi ni Yawe, Mungu wako, niliyekutoa katika inchi ya Misri, ambako ulikuwa mutumwa. “Usikuwe na miungu mingine isipokuwa mimi. “Usijifanyie sanamu za miungu, wala mufano wa kitu chochote kinachokuwa juu mbinguni, wala kinachokuwa chini katika dunia, wala kinachokuwa ndani ya maji chini ya dunia. Usiiname mbele yao wala kuvitumikia, kwa sababu mimi Yawe, Mungu wako, ni Mungu mwenye wivu. Ninawaazibu wana kwa ajili ya maovu ya baba zao, hata kizazi cha tatu na cha ine cha wale wanaonichukia. Lakini ninawatendea mema maelfu ya wale wanaonipenda na kushika amri zangu. “Usitaje bure jina langu mimi Yawe, Mungu wako, maana mimi Yawe sitaacha kumwazibu yeyote anayetaja bure jina langu. “Shika siku ya Sabato na kuitakasa, kama vile mimi Yawe, Mungu wako, nilivyokuamuru. Siku sita fanya kazi na tenda mambo yako yote. Lakini siku ya saba ni Sabato ya Yawe, Mungu wako. Siku hiyo usifanye kazi yoyote, wewe, wala mwana wako, wala binti yako, wala mutumwa wako, wala mujakazi wako, wala ngombe wako, wala punda wako, wala nyama wako yeyote, wala mugeni anayekuwa katika nyumba yako, kusudi mutumwa wako na mujakazi wako wapate kupumzika vilevile kama vile wewe. Usisahau kwamba wewe ulikuwa mutumwa katika inchi ya Misri, nami Yawe, Mungu wako, nikakutoa huko kwa mukono wenye nguvu na mukono ulionyooshwa. Ndiyo maana mimi Yawe, Mungu wako, nimekuamuru kushika siku ya Sabato. “Uheshimu baba yako na mama yako, kama vile mimi Yawe, Mungu wako, nilivyokuamuru, kusudi uishi maisha marefu na kufanikiwa katika inchi ninayokupatia mimi Yawe, Mungu wako. “Usiue. “Usizini. “Usiibe. “Usimushuhudie mwenzako uongo. “Usimutamani muke wa mwenzako, wala nyumba yake, wala shamba lake, wala mutumwa wake au mujakazi wake, wala ngombe wake, wala punda wake, wala kitu chochote mwenzako anachokuwa nacho.” “Hizi ndizo amri Yawe alizowaambia ninyi wote kwa sauti kubwa kutoka katika moto na lile wingu zito na giza nene, mulipokuwa mumekusanyika kule kwenye mulima. Hakuongeza hapo amri ingine. Kisha akaandika juu ya vibao viwili vya mawe, akanipatia. “Wakati muliposikia hiyo sauti kutoka katikati ya lile giza, juu ya ule mulima uliokuwa unawaka moto, viongozi wote wa makabila yenu na wazee walinifikia wakasema: ‘Sikiliza! Yawe, Mungu wetu, ametufunulia utukufu na ukubwa wake. Tumeisikia sauti yake kutoka katikati ya ule moto. Leo hivi tumemwona Mungu akisema na mwanadamu, naye mwanadamu pahali pa kufa akaendelea kuishi! Lakini kwa nini kujitia katika hatari ya kufa kwa kuteketezwa na ule moto mukubwa? Tukisikia tena sauti ya Yawe, Mungu wetu tutakufa! Ni mwanadamu gani aliyepata kusikia sauti ya Mungu Mwenye Uzima kutoka katikati ya moto kama vile tulivyomusikia sisi halafu akaweza kubaki muzima? Heri wewe Musa uende karibu, usikilize yote Yawe, Mungu wetu, atakayosema, kisha ukuje kutuambia mambo hayo yote atakayokuambia. Sisi tutayasikiliza na kuyatimiza’. “Bwana akasikia hayo maneno yenu, akaniambia: ‘Nimesikia maneno watu hawa waliyokuambia. Yote waliyosema ni sawa. Heri wangekuwa siku zote na mawazo kama haya wakiniheshimu na kushika amri zangu! Mambo yao yote yangewaendekea vizuri, wao wenyewe na wazao wao milele. Kwenda uwaambie warudi ndani ya mahema yao. Lakini wewe Musa usimame hapa karibu nami. Mimi nitakuambia amri zote na masharti na maagizo ambayo utawafundisha, kusudi inchi ambayo ninawapa ikuwe mali yao.’ “Ninyi mukuwe waangalifu mufanye kama vile Yawe alivyowaamuru. Mutimize kila kitu sawasawa. Mutafuata njia yote Yawe, Mungu wenu, aliyowaamuru kufuata kusudi mambo yenu yawaendekee vizuri na mupate kuishi muda murefu katika inchi mutakayotwaa ikuwe mali yenu. “Hii ndiyo amri, masharti na maagizo ambayo Yawe, Mungu wenu, aliniamuru niwafundishe, kusudi muyatimize katika inchi munayokwenda kuirizi. Wakati wote munapokuwa wazima, mutapaswa kumwogopa Yawe, Mungu wenu, na kutii masharti yote na amri ninazowapa ninyi na wazao wenu kusudi mupate kuishi maisha marefu. Kwa hiyo enyi Waisraeli, mukuwe waangalifu kwa kuzitimiza, kusudi mufanikiwe na kuongezeka sana katika inchi hiyo inayotiririka maziwa na asali kama vile alivyowaahidi. “Basi musikilize, enyi Waisraeli! Yawe, Yawe tu, ni Mungu wetu. Mumupende Yawe, Mungu wenu, kwa moyo wenu wote, kwa roho yenu yote na kwa nguvu yenu yote. Muweke ndani ya moyo wenu maneno hayo ninayowaamuru leo na kuwafundisha kwa uangalifu watoto wenu. Mutawaelezea mutakapokuwa munakaa katika nyumba au munapokuwa katika safari au munapolala au munapoamuka. Muyafunge katika mikono yenu na kuyavaa katika paji za nyuso zenu kama vile ukumbusho. Muyaandike kwenye miimo ya milango yenu na milango ya miji yenu. “Kama vile Yawe, Mungu wenu, alivyowaapia babu zenu, Abrahamu, Isaka na Yakobo, yeye atawapa inchi yenye miji mikubwa na mizuri iliyostawi ambayo ninyi hamukuijenga. Nyumba zitakuwa zimejaa vitu vizuri ambavyo ninyi hamukuviweka, kutakuwa visima ambavyo hamukuchimba na mashamba ya mizabibu na mizeituni ambayo hamukuyapanda. Yawe atakapowapeleka kwenye inchi hiyo ambako mutakuwa na chakula chote munachohitaji, muhakikishe kwamba hamutamusahau Yawe aliyewatoa Misri ambako mulikuwa watumwa. Mutamwogopa Yawe, Mungu wenu, mutamutumikia yeye peke yake na kuapa katika jina lake peke yake. Musiabudu miungu mingine, miungu ya watu wanaokuwa jirani nanyi, hasira ya Yawe isiwake juu yenu, naye asiwafute katika dunia, maana Yawe, Mungu wenu, anayekuwa kati yenu, ni Mungu mwenye wivu. “Musimujaribu Yawe, Mungu wenu, kama vile mulivyomujaribu huko Masa. Muhakikishe kwamba munatii amri, maagizo, na masharti ya Yawe, Mungu wenu, ambayo amewaamuru. Mufanye yale yanayomupendeza Yawe, kusudi mupate kufanikiwa. Mutaweza kuirizi inchi ile nzuri ambayo Yawe aliapa kuwapa babu zenu, na mutawafukuza waadui zenu kama vile Yawe alivyoahidi. “Siku zinazokuja, mwana wako atakapokuuliza: ‘Maana ya maagizo, masharti na maamuzi ambayo Yawe, Mungu wetu, aliwaamuru kutenda ni nini?’ Ninyi mutawajibu hivi: ‘Sisi tulikuwa watumwa wa mufalme wa Misri, na Yawe akatuokoa kwa mukono wake wenye nguvu. Kwa macho yetu wenyewe tulimwona akifanya vitambulisho na miujiza na mambo ya kutisha na ya ajabu juu ya Wamisri, mufalme wao na wakubwa wake. Alitutoa Misri, akatuleta hapa na kutupa inchi hii, kama vile alivyoapa kwamba atawapa babu zetu. Basi, Yawe akatuamuru kutii masharti haya yote na kumwogopa kwa faida yetu wenyewe, apate kutulinda siku zote kama hivi leo. Tukiwa waangalifu tukitimiza amri zote mbele ya Yawe, Mungu wetu, kama vile alivyotuamuru, tutahesabiwa kuwa wenye haki’. “Yawe, Mungu wenu atawafikisha kwenye inchi ambayo mutakwenda kufanya makao yenu na atafukuza mataifa mengi kutoka inchi hiyo. Mutakapoingia, atafukuza mbele yenu mataifa saba makubwa na yenye nguvu kuliko ninyi: Wahiti, Wagirgasi, Waamori, Wakanana, Waperizi, Wahivi, na Wayebusi. Vilevile, kisha Yawe, Mungu wenu, kuyatia katika mikono yenu, mutayashinda na kuyaangamiza kabisa. Musifanye agano lolote nayo wala musiyahurumie. Musioane nayo, wala musiyaoeshee wabinti zenu au wana wenu. Mukifanya hivyo wao watawapotosha watoto wenu wasimufuate Yawe, na kuwafanya waabudu miungu mingine, nayo hasira ya Yawe itawaka juu yenu, halafu atawaangamiza mara moja. Lakini muwatendee hivi: Mutavunja mazabahu zao na kubomoa nguzo zao. Na sanamu za Ashera mutakata na kuchoma sanamu zao za kuchonga. Mufanye hivyo kwa sababu ninyi mumetakaswa kwa Yawe, Mungu wenu. Kati ya watu wote katika ulimwengu aliwachagua ninyi kusudi mukuwe taifa lake mwenyewe. “Yawe hakuwapenda ninyi na kuwachagua kwa sababu ninyi ni wengi sana kuliko watu wengine; ninyi mulikuwa wachache kuliko mataifa mengine katika dunia. Lakini ni kwa sababu Yawe anawapenda na anashika kiapo alichowaapia babu zenu, ndiyo maana aliwaokoa kwa nguvu zake kubwa na kuwaokoa toka katika utumwa, toka mikono ya mufalme wa Misri. Basi, mujue kwamba Yawe, Mungu wenu, ndiye Mungu. Yeye ni Mungu mwaminifu, anayeshika agano lake na kutenda mema kwa vizazi vingi vya wale wanaomupenda na kushika amri zake. Lakini hatasita kuwaazibu wale wanaomuchukia. Kwa hiyo mukuwe waangalifu kushika amri, masharti na maagizo ninayowaamuru leo. “Mukisikiliza maagizo haya na kuyashika hata kuyatenda, Yawe, Mungu wenu, atashika agano lake nanyi na kuwatendea mema kama vile alivyowaahidi babu zenu. Atawapenda na kuwabariki, nanyi mutaongezeka na kuwa na wazao wengi. Atabariki mashamba yenu kusudi mupate ngano, divai na mafuta. Atawabariki kwa kuwapa ngombe na kondoo wengi katika inchi aliyowaahidi babu zenu kwamba atawapa ninyi. Mutabarikiwa kuliko watu wengine wote katika ulimwengu. Kati yenu hakutakuwa mwanaume wala mwanamuke tasa. Yawe atawaondolea magonjwa yote na hamutapatwa na magonjwa yoyote ya kutisha kama yaliyowapata huko Misri, lakini atawapa waadui zenu magonjwa hayo. Muangamize taifa lolote ambalo Yawe, Mungu wenu atalitia katika mikono yenu, wala musilionee huruma. Musiabudu miungu yao, maana jambo hili litakuwa mutego kwenu. “Musijisemeshe ndani mioyo yenu: ‘Watu hawa ni wengi kuliko sisi, tunaweza namna gani kuwafukuza toka katika inchi?’ Musiwaogope, mukumbuke vile Yawe, Mungu wenu, alivyomutendea mufalme wa Misri na inchi nzima ya Misri. Mukumbuke ugonjwa mukali muliouona kwa macho yenu, miujiza na maajabu na nguvu kubwa na uwezo mukubwa, ambavyo Yawe, Mungu wenu alitumia kwa kuwakomboa; vile ndivyo atakavyowatendea watu munaowaogopa. Zaidi ya hayo, Yawe, Mungu wenu, atatuma nyuki kati yao na kuwaangamiza wale ambao watawatoroka kwa kujificha. Basi, musiwaogope, kwa sababu Yawe, Mungu wenu, yuko kati yenu. Yeye ni Mungu mukubwa na wa kutisha. Yawe, Mungu wenu, atafukuza mataifa haya kadiri munavyosonga mbele kidogokidogo. Hamutaweza kuyaangamiza yote kwa mara moja, kwa sababu mukifanya hivyo hesabu ya nyama wa pori itazidi na kuwa kitisho kwenu. Yawe, Mungu wenu, atawatia waadui zenu katika mikono yenu na atawafanya wahangaike mpaka waangamie. Atawatia wafalme wao katika mikono yenu. Mutawaua, nao watasahaulika. Hakuna mutu yeyote atakayeweza kuwazuia, mpaka mutakapowaangamiza. Muteketeze kwa moto sanamu za miungu yao. Musitamani feza wala zahabu yao, wala musiitwae na kuifanya mali yenu. Kufanya hivyo ni mutego kwenu na ni chukizo kwa Yawe, Mungu wenu. Musipeleke sanamu zozote katika nyumba zenu, kama sivyo, mutalaaniwa kama sanamu hizo. Muzichukie na kuzizarau kwa sababu ni vitu vilivyolaaniwa. “Mutakuwa waangalifu kwa kutenda amri zote ninazowapa leo, kusudi mupate kuishi na kuongezeka, na muingie na kuirizi inchi ile ambayo Yawe aliapa kuwapa babu zenu. Mukumbuke jinsi Yawe, Mungu wenu, alivyowaongoza katika safari ndefu kupitia katika jangwa kwa muda wa miaka hiyo makumi ine, kusudi awanyenyekeze na kuwajaribu kusudi ajue yanayokuwa ndani ya mioyo yenu, na kama mungeshika amri zake au hapana. Aliwazarau akawaacha muone njaa na kisha akawapa mana mukule, chakula ambacho hamukukijua, wala babu zenu hawajapata kukijua. Alifanya hivyo kusudi apate kuwafundisha kwamba mwanadamu haishi kwa mukate tu, lakini kwa kila neno Yawe analosema. Wakati huo wa miaka makumi ine nguo zenu hazikuchakaa, wala miguu yenu haikuvimba. Mukumbuke kwamba Yawe, Mungu wenu, anawaazibu kama vile baba anavyoazibu mwana wake. Hivyo, mushike amri za Yawe, Mungu wenu, mupate kufuata njia zake na kumwogopa yeye. Yawe, Mungu wenu, anawaleta kwenye inchi nzuri, inchi yenye vijito na chemichemi, na maji yanayobubujika kutoka bonde na milima; inchi yenye ngano na shayiri, mizabibu, mitini, mikomamanga, mizeituni na asali. Huko mutapata chakula tele na hamutapungukiwa kitu. Mawe yake yana chuma, na kwenye milima yake munaweza kuchimba shaba. Mutakula na kushiba, mutamushukuru Yawe, Mungu wenu, kwa inchi nzuri aliyowapa. “Muhakikishe kwamba hamutamusahau Yawe, Mungu wenu, kwa kutoshika amri zake, maagizo yake na masharti yake ninayowaamuru leo. Mukisha kula na kushiba, kujijengea nyumba nzuri na kuishi humo, na wakati ambapo ngombe na kondoo wenu, zahabu na feza yenu, na kila kitu munachokuwa nacho kitakuwa kimeongezeka, musikuwe na kiburi na kumusahau Yawe, Mungu wenu, aliyewatoa katika inchi ya Misri, pahali mulipokuwa watumwa. Ni yeye aliyewaongoza katika lile jangwa kubwa na la kutisha, lenye nyoka wenye sumu na nge katika inchi ile yenye kukauka isiyokuwa na maji, aliwatolea maji kutoka kwenye jiwe gumu. Tena ni yeye aliyewakulisha mana katika jangwa, chakula ambacho babu zenu hawajapata kukijua. Alifanya hayo yote kusudi awanyenyekeze na kuwajaribu kwa kuwapima apate kuwajalia mema kwa mwisho. Hivyo mufanye angalisho kusudi musijisemeshe ndani ya mioyo yenu: ‘Tumejitajirisha kwa uwezo na nguvu zetu wenyewe’. Mukumbuke kwamba Yawe, Mungu wenu, ndiye anayewapa uwezo wa kupata utajiri. Anafanya hivyo kwa kuimarisha agano alilofanya na babu zenu mpaka leo. Lakini mukimusahau Yawe, Mungu wenu, na kufuata miungu mingine kwa kuitumikia na kuiabudu, ninawaonya vikali leo hii kwamba hakika mutaangamia. Musipomutii Yawe, mutaangamia kama vile mataifa ambayo anayaangamiza mbele yenu. “Musikilize enyi Waisraeli! Hivi leo mumekaribia kuvuka muto Yordani, kwenda kurizi inchi ya mataifa makubwa na yenye nguvu kuliko ninyi. Miji yao ni mikubwa na ina kuta zinazofika katika mawingu. Watu wenyewe ni warefu na wenye nguvu; ni Waanaki ambao kama vile munavyojua na kama vile mulivyosikia watu wanasema juu yao: ‘Nani anayeweza kuwashambulia?’ Mujue leo hii kwamba anayewatangulia kama vile moto unaoteketeza miti ni Yawe, Mungu wenu. Atawaangamiza na kuwashinda mbele yenu, kwa hiyo mutawafukuza na kuwaangamiza mara moja, kama vile Yawe alivyowaahidi. “Yawe, Mungu wenu akiacha kuwafukuza watu hao mbele yenu, musiseme ndani ya moyo wenu kwamba: ‘Ni kwa sababu ya uhaki wetu Yawe ametuleta tuirizi inchi hii’, ambapo Yawe amewafukuza watu hawa mbele yenu kwa sababu wao ni waovu. Munaweza kuirizi inchi yao si kwa sababu ninyi ni watu wa haki wenye mioyo ya usawa; lakini Yawe, Mungu wenu, anawafukuza watu hao mbele yenu kwa sababu ni waovu na anataka kuweka imara lile neno alilowaapia babu zenu, Abrahamu, Isaka na Yakobo. Basi, mujue kwamba Yawe, Mungu wenu, anawapa inchi hii nzuri muirizi si kwa sababu munastahili kuirizi, maana ninyi ni watu wagumu. “Mukumbuke na musisahau jinsi mulivyomukasirikisha Yawe, Mungu wenu, kule katika jangwa. Tangu siku ile mulipotoka katika inchi ya Misri mpaka siku mulipofika pahali hapa, ninyi mumekuwa mukimwasi Yawe. Hata huko kwenye mulima Horebu, mulimukasirikisha Yawe, naye alikasirika sana, kiasi cha kutaka kuwaangamiza. Nilipopanda juu ya mulima kupokea vibao vya mawe ambavyo kuliandikwa agano ambalo Yawe alifanya nanyi, nilikaa huko siku makumi ine, usiku na muchana; sikukula wala kunywa chochote. Kisha Yawe akanipa vibao viwili vya mawe vilivyoandikwa kwa kidole cha Mungu. Vilikuwa vimeandikwa maneno yote ambayo Yawe aliwaambia kwenye mulima kutoka kwenye moto siku ya mukutano. Hakika, nyuma ya siku hizo makumi ine, usiku na muchana, Yawe akanipa vibao hivyo viwili vya mawe ambavyo kuliandikwa agano. “Basi, Yawe akaniambia: ‘Ondoka, ushuke chini ya mulima upesi, kwa sababu watu wako uliowatoa Misri wamepotoka. Wameacha upesi njia niliyowaamuru wafuate na wamejifanyia sanamu ya kuyeyushwa’. “Vilevile, Yawe akaniambia: ‘Nimewaona watu hawa, ni watu wagumu sana. Uniache niwaangamize, nifute jina lao toka katika dunia. Nami nitakufanya wewe kuwa taifa lenye nguvu na kubwa kuliko wao.’ “Basi, nikageuka, nikashuka kutoka kwenye mulima, nikiwa nimebeba vile vibao viwili vya agano, nao moto ulikuwa unawaka juu ya mulima. Niliangalia, nikaona kwamba mumekwisha kutenda zambi mbele ya Yawe, Mungu wenu. Mulikwisha kujitengenezea sanamu ya mwana-ngombe ya kuyeyushwa. Bila kukawia mulikwisha kuacha njia ya Yawe ambayo aliwaamuru. Hivyo, nikashika vile vibao viwili nikavitupa chini, nikavivunja mbele yenu. Kisha nikalala uso mpaka chini mbele ya Yawe, kama vile mbele, kwa muda wa siku makumi ine usiku na muchana. Sikukula chakula wala kunywa maji, kwa sababu ya zambi muliyokuwa mumetenda kwa kufanya maovu mbele ya Yawe kwa kumukasirikisha. Niliogopa kwamba hasira na kasirani ya Yawe juu yenu ingewaangamiza, lakini Yawe akanisikiliza vilevile wakati huo. Yawe alikuwa amemukasirikia sana Haruni, kiasi cha kumwangamiza. Hivyo, nikamwombea Haruni wakati huohuo. Kile kitu kiovu, ni kusema yule mwana-ngombe muliyejitengenezea, nilikitwaa, nikakiteketeza ndani ya moto, nikakipondaponda na kukisagasaga, kikakuwa mavumbi laini. Halafu nikayatupa hayo mavumbi kwenye kijito kilichotiririka chini ya mulima huo. “Tena mulimukasirikisha Yawe, Mungu wenu, huko Tabera, Masa na Kiburoti-Hatawa. Na Yawe alipowatuma kutoka Kadesi-Barnea, akisema ‘Muende murizi inchi ambayo nimewapatia’, hamukufuata amri ya Yawe, Mungu wenu. Hamukuamini wala hamukutii yale aliyowaambia. Ninyi mumekuwa waasi mbele ya Yawe tangu siku nilipowajua. “Kwa hiyo, nikalala uso mpaka chini mbele ya Yawe siku hizo makumi ine, usiku na muchana, kwa sababu Yawe alikuwa amesema atawaangamiza. Nikamwomba Yawe, nikisema: Ee Yawe, usiwaangamize watu wako na urizi wako, watu uliowakomboa na kuwatoa katika inchi ya Misri kwa uwezo na nguvu yako kubwa. Uwakumbuke watumishi wako, Abrahamu, Isaka na Yakobo, wala usijali ugumu, uovu na zambi za watu hawa. Watu wa kule ulikotutoa wasiseme: ‘Yawe aliwatoa kusudi awaue katika jangwa kwa sababu hakuweza kuwaingiza katika inchi aliyowaahidi na kwa sababu aliwachukia’. Maana, hawa ni watu na urizi wako, watu ambao uliwatoa kwa nguvu na uwezo wako mukubwa. “Kisha Yawe akaniambia: ‘Chonga vibao viwili vya mawe kama vile vya kwanza, na sanduku la mbao. Kuja kwangu huku juu kwenye mulima, nami nitaandika maneno yaliyokuwa yameandikwa katika vibao vile ulivyovunja, kisha uweke vibao hivyo katika sanduku’. “Basi, nikatengeneza sanduku la mushita na vibao viwili vya mawe kama vile vya kwanza, nikavitwaa katika mukono, nikapanda navyo kwenye mulima. Yawe akaandika katika vibao hivyo maneno kama yaleyale ya kwanza: amri kumi ambazo aliwapa aliposema kutoka katika moto siku ya mukutano. Halafu Yawe akanipa vibao hivyo. Nikageuka, nikashuka kutoka kwenye mulima, nikaweka vibao hivyo ndani ya sanduku nililokuwa nimetengeneza, na vimo ndani ya sanduku hilo, kama vile Yawe alivyoniamuru.” (Watu wa Israeli wakasafiri kutoka visima vya watu wa Yakani mpaka Musara. Haruni akakufa na kuzikwa kule. Eleazari mwana wake, akatwaa nafasi yake kama vile kuhani. Kutoka pale, wakasafiri mpaka Gudigoda, na kutoka Gudigoda mpaka Yotibata, eneo lenye vijito vingi vya maji. Wakati huo, Yawe akachagua watu wa kabila la Lawi wakuwe wanabeba Sanduku la Agano la Yawe, wamutumikie kama vile makuhani na kubariki watu kwa jina lake hata hivi leo. Ndiyo maana kabila la watu wa Lawi halina sehemu ya inchi ya urizi pamoja na wandugu zao. Walichopokea ni heshima ya kuwa makuhani wa Yawe, kama vile Yawe, Mungu wenu, alivyoahidi.) “Nikakaa kwenye mulima kwa muda wa siku makumi ine, usiku na muchana, kama vile mbele. Yawe akanisikiliza kwa mara ingine tena na akakubali kutowaangamiza. Kisha akaniambia: ‘Ondoka uendelee na safari yako ukiwaongoza watu kusudi waweze kuingia na kurizi inchi niliyowaapia babu zenu kwamba nitawapa’. “Sasa, enyi Waisraeli, Yawe, Mungu wenu, anataka nini kwenu? Yawe, Mungu wenu, anataka mumwogope, mufuate njia zake zote, mumupende, mumutumikie Yawe, Mungu wenu, kwa moyo wote na kwa roho yenu yote, na mutii amri na masharti ya Yawe ninayowawekea leo, kwa mafaa yenu wenyewe. Angalia, mbingu hata mbingu za mbingu ni mali ya Yawe, Mungu wenu, dunia na vyote vinavyokuwa ndani yake. Tena Yawe alifurahia babu zenu kwa kuwapenda na akawachagua ninyi wazao wao pahali pa watu wengine wote, kama hivi leo. Kwa hiyo, mutahiri magovi ya mioyo yenu, musikuwe wagumu tena. Maana Yawe, Mungu wenu, ndiye Mungu wa miungu na Bwana wa wabwana. Yeye ni Mungu mukubwa na mwenye nguvu, na wa kuogopesha. Hapendelei wala hapokei kituliro. Anatetea haki ya wayatima na wajane; vilevile anawapenda wageni na kuwapa chakula na nguo. Basi, muwapende wageni kwa sababu nanyi vilevile mulikuwa wageni katika inchi ya Misri. Mumwogope Yawe, Mungu wenu, mumutumikie, muambatane naye na kuapa kwa jina lake. Yeye ni utukufu wenu. Yeye ni Mungu wenu ambaye amewatendea haya mambo makubwa na ya kutisha muliyoona kwa macho yenu wenyewe. Babu zenu walipokwenda Misri, walikuwa watu makumi saba tu, lakini sasa Yawe, Mungu wenu, amewafanya kuwa wengi kama nyota mbinguni. “Mumupende Yawe, Mungu wenu, na kushika siku zote masharti yake, maagizo yake na amri zake. Mufikiri kwa uangalifu, kwa sababu ya watoto wenu ambao hawakujua wala hawakuona azabu ya Yawe, uwezo wake na nguvu zake, vitambulisho vyake na maajabu yake aliyotenda kule Misri kwa mufalme wa Misri na inchi yake yote, aliyotendea jeshi la Misri, farasi wao na magari yao ya vita, jinsi alivyozamisha jeshi hilo katika bahari Nyekundu, na jinsi Yawe alivyoliangamiza hata hivi leo. Mukumbuke jinsi Yawe aliyowafanyia ninyi katika jangwa mbele hamujafika hapa, na mambo aliyowatendea Datani na Abiramu, wana wa Eliabu, mwana wa Rubeni. Mukumbuke jinsi mbele ya watu wote wa Israeli udongo ulivyofunguka na kuwameza pamoja na jamaa zao, mahema yao, nyama na watumishi wao wote. Maana macho yenu yameona matendo yote haya makubwa ambayo Yawe alifanya. “Mutii amri zote ninazowaamuru siku hii ya leo, kusudi mupate kuingia na kurizi inchi munayoiendea, mupate kuishi kwa muda murefu katika inchi inayotiririka maziwa na asali, inchi ambayo Yawe aliahidi kuwapa babu zenu na wazao wao. Inchi munayokwenda kurizi si kama inchi ya Misri mulikotoka, ambako mulipanda ngano nanyi mulipaswa kuleta maji kutoka kwenye mito kwa kuimwangilia kama vile mulivyofanya kwa mashamba ya mboga. Lakini inchi munayokwenda kurizi ni inchi ya milima na mabonde, inchi ambayo inapata maji ya mvua kutoka mbinguni, inchi ambayo Yawe, Mungu wenu, anatunza. Siku zote anaiangalia tangu mwanzo wa mwaka hata mwisho wa mwaka. “Basi, mukitii amri zangu ninazowapa leo, mukimupenda Yawe, Mungu wenu, na kumutumikia kwa moyo wenu wote na kwa roho yenu yote, yeye ataipatia inchi yenu mvua wakati wake, mvua za kwanza na mvua za mwisho, nanyi mutavuna ngano yenu, divai yenu na mafuta yenu. Ataotesha majani katika mashamba kwa ajili ya ngombe wenu, nanyi mutakula na kushiba. Mufanye angalisho kusudi mioyo yenu isidanganywe, mukigeuka na kutumikia miungu mingine na kuiabudu, nayo hasira ya Yawe iwake juu yenu, naye afunge mbingu hata kusikuwe mvua, na inchi iache kutoa mazao yake, halafu muangamie upesi kutoka katika inchi nzuri ambayo Yawe anawapa. “Muweke maneno yangu haya ndani ya mioyo yenu na roho zenu. Muyafungie katika mikono yenu kama vile kitambulisho na kuyavaa katika paji la uso. Muwafundishe watoto wenu maneno haya mukiyazungumuzia munapoikaa katika nyumba zenu, munapotembea, munapolala na munapoamuka. Muyaandike kwenye miimo ya milango yenu na milango ya miji yenu, kusudi ninyi na watoto wenu mupate kuishi maisha marefu katika inchi ambayo Yawe, Mungu wenu, aliapa kuwapa babu zenu, siku zote mbingu zitakapodumu juu ya dunia. “Kama mukishika amri zote ambazo nimewapa, mukimupenda Yawe, Mungu wenu, na kufuata njia zake zote na kuambatana naye, basi Yawe atafukuza mataifa yote hayo mbele yenu, nanyi mutarizi inchi inayokuwa mali ya mataifa makubwa na yenye nguvu kuliko ninyi. Kila pahali mutakapokanyaga kwa miguu yenu patakuwa penu. Inchi yenu itaenea kutoka katika jangwa, upande wa kusini, mpaka kwenye milima ya Lebanoni upande wa kaskazini, na kutoka muto Furati upande wa mashariki, mpaka kwenye bahari ya Mediteranea upande wa magaribi. Hakuna mutu yeyote atakayeweza kuwashambulia. Popote mutakapokwenda katika inchi hiyo, Yawe, Mungu wenu, atawatia watu hofu wawaogope, kama vile alivyowaahidi. “Leo hii ninawawekea mbele yenu baraka na laana: baraka, kama mutatii amri za Yawe, Mungu wenu, ambazo ninawapa hivi leo; na laana, kama hamutatii amri za Yawe, Mungu wenu, na kuacha njia ninayowaamuru, mukiabudu miungu mingine ambayo hata hamujajua bado. Yawe atakapowafikisha kwenye inchi munayokwenda kurizi, mutatangaza baraka kutoka kwenye mulima Gerizimu, na laana kutoka kwenye mulima Ebali. (Milima hii iko ngambo ya muto Yordani, upande wa magaribi wa barabara kuelekea upande jua linakotokea, katika inchi ya Wakanana wanaoishi Araba kuelekea Gilgali.) Maana mutavuka muto Yordani muingie kwa kurizi inchi ambayo Yawe, Mungu wenu, anawapa. Basi mutakapoirizi na kukaa humo, muangalie kwamba munatimiza masharti yote na maagizo ambayo ninawapa leo. “Haya ndiyo masharti na maagizo ambayo mutatimiza katika inchi ambayo Yawe, Mungu wa babu zenu amewapa kwa kuirizi, siku zote za kuishi kwenu juu ya inchi. Muharibu kabisa pahali pote ambapo watu wanaabudia miungu yao kwenye milima mirefu, vilima na chini ya miti yenye majani mabichi. Muvunje mazabahu zao, na kubomoa kabisa nguzo zao. Muteketeze kwa moto sanamu zao za Ashera na kukatakata sanamu zao za kuchonga na kufuta kabisa jina lao na pahali hapo. “Wala musimwabudu Yawe, Mungu wenu, namna hiyo yao. Lakini mutakwenda pahali ambapo Yawe, Mungu wenu, atachagua katika makabila yote kwa kuweka jina lake na makao yake hapo. Huko ndiko mutakakokwenda. Vilevile huko mutapeleka sadaka zenu za kuteketezwa kwa moto na sadaka zingine, sehemu ya kumi za mazao yenu, matoleo yenu ya mapenzi na ya kutimiza kiapo, na wazaliwa wa kwanza wa ngombe na kondoo wenu. Huko, mutakula mbele ya Yawe, Mungu wenu, na mutafurahi ninyi pamoja na watu wa nyumba zenu kwa ajili ya mafanikio yenu Yawe, Mungu wenu, aliyowabarikia. “Musifanye kama vile tunavyofanya sasa, kila mutu kama vile anavyopenda mwenyewe; kwa sababu bado hamujaingia pahali pa kupumzikia na katika urizi Yawe, Mungu wenu, anaowapa. Lakini mutakapovuka muto Yordani na kuishi katika inchi ambayo Yawe, Mungu wenu, atawapatia muirizi, na atakapowapatia pumziko musisumbuliwe na waadui zenu wote watakaowazunguka kusudi mupate kuishi salama, basi huko pahali Yawe, Mungu wenu, atakapochagua kusudi jina lake likae pale, hapo mutapeleka yote ninayowaamuru: sadaka zenu za kuteketeza kwa moto na sadaka zingine, sehemu ya kumi za mazao yenu, na sadaka za kutimiza kiapo. Huko mutafurahi mbele ya Yawe, Mungu wenu, ninyi pamoja na watoto wenu wanaume na wanawake, watumishi na wajakazi wenu, na Walawi wanaoishi kati yenu kwa sababu hawana sehemu wala urizi kati yenu. Mufanye angalisho musitoe sadaka zenu za kuteketezwa pahali popote munapoona; lakini pahali ambapo Yawe atakapopachagua katika kabila moja kati ya makabila yenu, hapo ndipo pahali mutakapotolea sadaka zenu za kuteketezwa na ni hapo mutakapofanyia mambo mengine yote ambayo nimewaamuru mufanye. “Lakini muna uhuru wa kuchinja na kula nyama wenu popote katika makao yenu munavyopenda, kama vile baraka za Yawe, Mungu wenu, alizowapa, kadiri mutakavyojaliwa na Yawe. Watu wote, wanaokuwa safi au wachafu wanaweza kula, kama vile munavyokula nyama ya paa au ya kulungu. Lakini musikule damu ya nyama hao; mumwange damu hiyo chini kama vile maji. Musikule vitu hivi pahali munapoishi: sehemu ya kumi za ngano zenu, divai zenu au mafuta yenu, wazaliwa wa kwanza wa ngombe wenu au kondoo wenu, au sadaka zenu za kutimiza kiapo au za mapenzi, au matoleo mengine. Mutavikula mbele ya Yawe, Mungu wenu, pahali Yawe, Mungu wenu, atakapochagua. Mutavikula ninyi pamoja na wana wenu na wabinti zenu, watumishi wenu na wajakazi wenu, na Walawi wanaoishi katika miji yenu. Vilevile muhakikishe kwamba hamutawasahau Walawi muda wote mutakaoishi katika inchi yenu. “Yawe, Mungu wenu atakapopanua inchi yenu, kama vile alivyoahidi, nanyi mutasema: ‘Tutakula nyama’ kwa sababu munapenda nyama, munaweza kula nyama kiasi munachotaka. Basi, pahali Yawe, Mungu wenu, atakapochagua, apaweke jina lake, hapo munaweza kuchinja ngombe au kondoo yeyote ambaye Yawe amewajalia, kama nilivyowaamuru na munaweza kula kiasi chochote munachotaka cha nyama hiyo, kama mukiwa katika miji yenu. Mutaikula nyama hiyo kama vile wanavyokula paa au kulungu. Mutu yeyote anaweza kula, anayekuwa safi na asiyekuwa safi. Lakini muhakikishe kwamba hamukuli damu, maana damu ni uzima. Hivyo basi, musikule uzima pamoja na nyama. Musikule damu hiyo, lakini muimwange chini kama vile maji. Musikule damu, nanyi mutafanikiwa pamoja na wazao wenu, maana mutakuwa munatenda kwa usawa mbele ya Yawe. Vitu vitakatifu mutakavyotoa na sadaka zenu za kutimiza kiapo, mutavitwaa na kuvipeleka pahali Yawe atakapochagua. Hapo, mutatoa sadaka za kuteketezwa, nyama na damu, kwenye mazabahu ya Yawe, Mungu wenu. Damu ya nyama mutainyunyiza kwenye mazabahu ya Yawe Mungu wenu, lakini munaruhusiwa kula nyama. Mufanye angalisho kutii maneno haya niliyowaamuru, kusudi mupate kufanikiwa ninyi pamoja na wazao wenu nyuma yenu milele, maana mutakuwa munatenda mazuri na kwa usawa mbele ya Yawe, Mungu wenu. “Yawe, Mungu wenu ataangamiza mataifa mbele yenu, hayo ambayo munakwenda kuyafukuza, kuyatoa na kukaa katika inchi yao. Atakapokwisha kuyaangamiza mbele yenu, mufanye angalisho musijiingize katika mutego kwa kuyafuata. Musijisumbue kujua kitu juu ya miungu yao, mukisema: ‘Mataifa haya yaliabudu namna gani miungu yake kusudi nasi tuwaabudu vile vile?’ Musimwabudu Yawe, Mungu wenu, hivyo, kwa maana kila chukizo ambalo Yawe hapendi, wameifanyia miungu yao, hata wamewachoma ndani ya moto watoto wao wanaume na wanawake, kwa kutambikia miungu yao. “Kila kitu ambacho nimewaamuru, mufanye angalisho mukitende; musiongeze kitu wala musipunguze kitu. “Kukitokea nabii au mutabiri wa kutumia ndoto kati yenu na kuwapatia kitambulisho au ajabu fulani, kisha neno, vitambulisho au maajabu aliyowaambia yakitokea, na akisema: ‘Tufuate miungu mingine, miungu ambayo hamujapata kuijua, na tuitumikie’, musisikilize maneno ya nabii huyo au mutabiri wa kutumia ndoto, kwa maana Yawe, Mungu wenu, anawatumia kwa kuwajaribu kusudi ajue kama munamupenda yeye Yawe, Mungu wenu, kwa moyo wenu wote na roho yenu yote. Mufuate na kumwogopa Yawe, Mungu wenu, na kushika amri zake na kutii sauti yake. Mumutumikie na kuambatana naye. Lakini nabii huyo au mutabiri wa kutumia ndoto atauawa, kwa sababu atakuwa amewafundisha uasi mbele ya Yawe, Mungu wenu, aliyewatoa katika inchi ya Misri na kuwakomboa kutoka katika utumwa, kusudi muache njia ambayo Yawe, Mungu wenu, aliwaamuru kufuata. Hivi ndivyo mutakavyokomesha uovu kati yenu. “Ikiwa ndugu yako wa tumbo moja, au mwana wako, au binti wako, au muke wako unayemupenda sana au rafiki yako mupenzi, atakushawishi kwa siri akisema: ‘Twende tuabudu miungu mingine’, ambayo wewe wala babu zenu hamwijui, miungu ya watu wanaoishi karibu nanyi au miungu ya watu wanaoishi mbali tokea incha moja ya dunia mpaka incha nyingine, usikubali kushawishiwa wala kumusikiliza, au kumuhurumia wala usimwachilie wala usimufiche; lakini utamwua. Mukono wako unapaswa ukuwe wa kwanza wakati wa kumwua halafu wengine wote watafuata vilevile. Umupige mawe mpaka akufe, kwa sababu amejaribu kukuvuta mbali kutoka kwa Yawe, Mungu wako, ambaye alikutoa toka utumwa katika inchi ya Misri. Hivyo, Waisraeli wote watasikia na kuogopa, na hawatafanya uovu kama huo hata kidogo. “Mutakapoishi katika miji ambayo Yawe, Mungu wenu anawapa, labda mutasikia kwamba watu fulani wa ovyo ovyo kati yenu, wamewashawishi watu wa muji wakisema: ‘Twende tuabudu miungu mingine’, ambayo bado hamukujua, basi mutapeleleza na kufanya uchunguzi na kuuliza kwa uangalifu. Na kama ni kweli kwamba jambo la kuchukiza limetendeka kati yenu, hakika mutawaua kwa upanga watu wa muji huo. Mutauteketeza kwa upanga kabisa na ngombe wote vilevile. Mutakusanya vitu vyote mulivyoteka katika kiwanja cha muji na kuchoma kwa moto vitu vile vyote kama vile sadaka ya kuteketezwa kwa ajili ya Yawe, Mungu wenu. Muji huo utakuwa lundo la mabomoko milele, nao hautajengwa tena. Kitu ambacho kimekwisha kutolewa kiteketezwe musikitwae, kusudi Yawe aache ile hasira yake mbaya. Yawe, Mungu wenu, atawaonyesha rehema na kuwafanya ninyi mukuwe wengi sana kama vile alivyoahidia babu zenu, kama tu mutatii sauti yake, mukishika amri zake zote ambazo ninawapa hivi leo na kufanya kile kinachokuwa sawa mbele yake. “Ninyi ni watoto wa Yawe, Mungu wenu; musijichanje wala kunyoa nywele upande wa mbele kwa ajili ya mutu aliyekufa. Ninyi ni watakatifu wa Yawe, Mungu wenu. Yawe amewachagua ninyi kuwa watu wake kati ya watu wote katika dunia yote. “Musikule kitu kinachokuwa chukizo kwa Mungu. Munaweza kula nyama hawa: ngombe, kondoo, mbuzi, kulungu, paa, kongoni, mbuzi wa pori, paa mweupe, pofu na mbuzi wa mulima, na kila nyama mwenye kwato zinazogawanyika sehemu mbili na mwenye kucheua. Lakini musikule nyama yeyote ambaye kwato zake hazigawanyiki sehemu mbili na hacheui. Musikule ngamia, sungura na pelele, ingawa wanacheua lakini kwato zao hazigawanyiki sehemu mbili; hao ni wachafu kwenu. Vilevile musikule nguruwe, maana ijapokuwa kwato zake zinagawanyika sehemu mbili, yeye hacheui; hao ni wachafu kwenu. Musikule nyama zao wala musiguse mizoga yao. “Munaweza kula kila aina ya samaki wenye mapezi na magamba. Lakini kiumbe chochote kinachoishi ndani ya maji kisichokuwa na mapezi wala magamba musikule; hivyo ni vichafu kwenu. “Munaweza kula ndege wote wanaokuwa safi. Lakini musikule ndege hawa: furukombe, kipungu, kengewa, kozi, mwewe na aina zake, kibombobombo na aina zake, mbuni, kirukanjia, dudumizi, kipanga na aina zake, bundi, mumbi, bundi mukubwa, mwari, nderi, munandi, membe, koikoi na aina zake, hudihudi na popo. Na wadudu wote wenye mabawa ni wachafu kwenu; musiwakule. Munaweza kula viumbe vyote vyenye mabawa vinavyokuwa safi. Musikule nyamafu yeyote lakini munaweza kumupa mugeni anayeishi katika miji yenu, akule, au munaweza kumwuzishia mutu wa taifa lingine. Musipike mwana-mbuzi katika maziwa ya mama yake. “Ninyi ni watakatifu na Yawe ni Mungu wenu. “Mutoe sehemu ya kumi ya mazao yenu yote ya shamba kila mwaka. Halafu muende pahali ambapo Yawe, Mungu wenu amepachagua kwa kuweka jina lake, na mukiwa mbele yake mutakula sehemu ya kumi ya ngano yenu, ya divai yenu na ya mafuta, na ya wazaliwa wa kwanza wa ngombe na kondoo wenu. Mufanye hivi kusudi mujifunze kumwogopa Yawe, Mungu wenu siku zote. Ikiwa safari ni ndefu kwa sababu Yawe, Mungu wenu, amechagua pahali pa kuweka jina lake ambapo ni mbali sana na nyumba, nanyi hamuwezi kubeba sehemu ya kumi za mazao yenu ambayo Yawe amewajalia kupata, basi, mufanye hivi: “Muuzishe mazao yenu na kupeleka feza hiyo mpaka pahali Yawe, Mungu wenu, alipochagua, muzitumie hizo feza kwa kitu chochote mutakachopenda - nyama ya ngombe, nyama ya kondoo, divai au kinywaji kikali. Mutavikula na kufurahi hapo mbele ya Yawe, Mungu wenu, pamoja na jamaa zenu. “Musiwasahau Walawi wanaoishi kati yenu; wao hawana fungu wala urizi wao kati yenu. Kila mwisho wa mwaka wa tatu mutoe sehemu ya kumi ya mazao yenu yote na kuyaweka akiba katika miji yenu. Hiyo itakuwa kwa ajili ya Walawi, kwa sababu hawana fungu wala urizi wao kati yenu, nao wageni, wayatima na wajane ambao wanaishi katika miji yenu, watakuja kula na kushiba. Mufanye hivi naye Yawe, Mungu wenu, atawabariki katika kazi zenu zote munazofanya kwa mikono yenu. “Kila mwisho wa mwaka wa saba mutawasamehe wote wenye kuwa na madeni yenu. Hivi ndivyo mutakavyofanya: kila mumoja aliyemukopesha mwenzake, afute lile deni, wala asijaribu kumudai kwa sababu Yawe mwenyewe ameamua deni hilo lifutwe. Munaweza kuwadai wageni, lakini madeni yote ya wandugu zenu wenyewe mutayafuta. “Yawe, Mungu wenu atawabariki katika inchi anayowapa ikuwe urizi wenu. Hakuna hata mumoja atakayekuwa masikini kati yenu, ikiwa tu mutamutii Yawe, Mungu wenu, kwa kufuata kwa uangalifu amri ninazowapa hivi leo. Yawe, Mungu wenu, atawabariki kama vile alivyowaahidi. Nanyi mutayakopesha mataifa mengi, lakini ninyi hamutakopa. Vilevile mutatawala mataifa mengi, lakini mataifa hayo hayatawatawala ninyi. “Kukiwa masikini wa jamaa yenu katika miji ya inchi ambayo Yawe atawapa, musikuwe wachoyo na wagumu kwake. Pahali pake, mufungue mikono yenu na kumukopesha kwa mapenzi kiasi cha kutosha mahitaji yake. Muangalie wazo ovu lisiwaingie ndani ya mioyo yenu, mukisema: ‘Mwaka wa saba, mwaka wa kusamehe wadeni uko karibu’. Mukimwangalia ndugu yenu masikini na jicho baya na kukataa kumupa chochote, yeye anaweza kumulilia Yawe juu yenu na hiyo itakuwa zambi kwenu. Mumupe ndugu masikini kwa moyo safi bila kunungunika, maana kwa ajili ya hayo, Yawe, Mungu wenu, atawabariki katika kazi zenu zote na katika kila munalofanya. Wamasikini hawatakosekana katika inchi; hivyo ninawaamuru, mukuwe wenye moyo safi kwa wandugu zenu wenye mahitaji na wamasikini katika inchi yenu. “Kama ndugu Mwebrania, mwanaume au mwanamuke, akiuzishwa kwako, atakutumikia kwa miaka sita, lakini katika mwaka wa saba, utamwacha huru. Nawe utakapomwacha huru, usimwache aende mikono mitupu. Umupe kwa moyo safi kile ambacho Yawe amekubariki nacho: kondoo, ngano na divai. Mukumbuke kwamba ninyi mulikuwa watumwa huko Misri na Yawe, Mungu wenu, aliwakomboa; ndiyo maana leo ninawaamuru hivyo. Lakini akikuambia: ‘Sitaondoka kwako’, kwa sababu anakupenda wewe na jamaa yako na anaishi vizuri kwako, basi, utatwaa chuma na kutoboa sikio lake mpaka chuma hicho kiingie ndani ya mulango naye atakuwa mutumwa wako milele. Utamutendea mujakazi wako namna hiyohiyo. Wala usione ugumu utakapomwacha huru mutumwa wako, maana, amekutumikia kwa muda wa miaka sita kwa nusu ya mushahara wa mutumishi wa kulipwa. Fanya hivyo, naye Yawe, Mungu wako, atakubariki kwa kila utakalofanya. “Umutolee Yawe, Mungu wako, wazaliwa wote wa kwanza dume wa kundi lako la ngombe na kondoo. Usiwafanyizishe ngombe hao kazi na kondoo hao usiwakate manyoya. Kila mwaka, wewe na jamaa yako mutakula nyama hao mbele ya Yawe, Mungu wenu, pahali Yawe atakapochagua. Lakini nyama huyo akiwa na kilema chochote, ni kusema kiwete au kipofu, au ana kilema chochote kikubwa, usimutoe kuwa sadaka kwa Yawe, Mungu wako. Utakula nyama wa namna hiyo ukiwa katika muji wako; vilevile wote wanaokuwa safi na wasiokuwa safi wanaweza kumukula kama vile unavyokula paa au kulungu. Lakini usikule damu yake; hiyo utaimwanga chini kama vile maji. “Mushike mwezi wa Abibu na kufanya Pasaka kwa heshima ya Yawe, Mungu wenu. Maana katika mwezi huo wa Abibu, Yawe, Mungu wenu aliwatoa Misri wakati wa usiku. Mutatoa sadaka ya Pasaka kutoka mifugo yenu ya kondoo au ngombe kwa heshima ya Yawe pahali ambapo Yawe atachagua kwa ajili ya jina lake. Musikule sadaka hiyo na mikate iliyotiwa chachu. Kwa muda wa siku saba mutakula mikate isiyotiwa chachu, nayo ni mikate ya mateso – kwa sababu mulitoka Misri kwa haraka; kwa hiyo, muda wote mutakaoishi mutakumbuka ile siku mulipotoka Misri. Kwa muda wa siku saba mutu yeyote katika inchi yenu asiweke chachu ndani ya nyumba yake, na nyama ya yule nyama aliyechinjwa magaribi ya siku ya kwanza isibaki mpaka asubui. Musitolee sadaka ya Pasaka katika muji wowote ambao Yawe, Mungu wenu, atawapa; lakini mutaitolea pale pahali Yawe, Mungu wenu, atakapochagua kwa ajili ya jina lake. Mutatolea sadaka ya Pasaka magaribi, jua linapotua, wakati uleule mulipotoka Misri. Hiyo nyama mutaipika na kuikula pahali pale Yawe, Mungu wenu atakapochagua. Asubui yake mutageuka na kurudi katika mahema zenu. Katika siku sita mutakula mikate isiyotiwa chachu. Katika siku ya saba kutakuwa mukutano mukubwa wa kumwabudu Yawe, na hamutafanya kazi yoyote katika siku hiyo. “Mutahesabu majuma saba; mutaanza kuyahesabu tangu munapoanza kuvuna ngano. Halafu mutafanya sikukuu ya majuma kwa heshima ya Yawe, Mungu wenu, kwa kutoa sadaka ya mapenzi kadiri Yawe, Mungu wenu, anavyowabariki. Mutafurahia mbele ya Yawe, Mungu wenu, ninyi pamoja na wana wenu na wabinti zenu, watumishi wenu, Walawi, wageni, wayatima na wajane ambao wanaishi pamoja nanyi. Mufanye haya katika pahali Yawe, Mungu wenu, atakapochagua kwa ajili ya jina lake. Mukumbuke kwamba mulikuwa watumwa kule Misri na mukuwe waangalifu kufuata masharti haya. “Kisha kupepeta ngano yenu yote na kukamua zabibu zenu, mutafanya sikukuu ya vibanda kwa muda wa siku saba. Mutafanya karamu hiyo, ninyi na watoto wenu wanaume na wanawake, watumishi wenu, Walawi, wageni, wayatima na wajane ambao wanaishi katika miji yenu. Kwa siku saba mutamufanyia Yawe, Mungu wenu, karamu pahali ambapo Yawe atachagua; kwa sababu Yawe, Mungu wenu atawabariki kwa mazao yenu yote na katika shuguli zenu zote nanyi hakika mutafurahi. “Wanaume wote wa taifa lenu watakuja mbele ya Yawe, Mungu wenu, mara tatu kila mwaka, pahali ambapo Yawe, Mungu wenu atachagua: wakati wa sikukuu ya Pasaka, sikukuu ya kuvuna na wakati wa sikukuu ya vibanda. Wasitokee mbele ya Yawe mikono mitupu. Wote watatoa kadiri wanavyoweza kulingana na baraka Yawe, Mungu wenu, alizowajalia. “Mutachagua waamuzi na wakubwa kutoka makabila yenu katika miji yenu ambayo Yawe, Mungu wenu, atawapa nao watatoa hukumu za haki kwa watu. Musipotoshe haki, musikuwe na upendeleo, wala musikubali kupokea kituliro, kwa kuwa kituliro kinapofusha macho ya watu wenye hekima na kupotosha maneno ya mutu mwenye haki. Mutafuata yanayokuwa ya haki tu, kusudi mupate kuishi na kurizi inchi munayopewa na Yawe, Mungu wenu. “Musipande muti wowote ukuwe nguzo ya mungu wa uongo karibu na mazabahu mutakayomujengea Yawe, Mungu wenu. Wala musisimamishe nguzo ambayo Yawe Mungu wenu anaichukia. “Musitoe sadaka kwa Yawe, Mungu wenu, ngombe au kondoo mwenye kilema; hiyo ni chukizo kwa Yawe, Mungu wenu. “Kama mukisikia katika mumoja wa miji yenu kuna mwanaume au mwanamuke anayetenda maovu mbele ya Yawe, Mungu wenu, na kuvunja agano lake naye amekwenda na kutumikia miungu mingine na kuiabudu, akiabudu jua, mwezi au vitu vingine vya mbinguni nisivyoagiza, mutafanya uchunguzi kamili, na kama ni kweli kwamba kitu hiki kiovu kimefanywa katika Israeli, basi, mumupeleke mutu huyo inje ya miji na kumupiga mawe mpaka akufe. Hata hivyo, atauawa ikiwa kuna ushuhuda wa watu wawili au watatu. Asiuawe ikiwa kuna ushuhuda wa mutu mumoja tu. Wale washuhuda ndio watakaoanza kumupiga mawe kwanza, halafu wengine wamupige mawe. Ndivyo mutakavyokomesha uovu kati yenu. Inawezekana kutatokea mashitaki mengine yanayokuwa magumu ndani ya miji yenu, kama vile maneno yanayoelekea uchafu, mambo ya haki za watu, na hasara ya mwili. Basi, mutaondoka na kwenda pahali Yawe, Mungu wenu alipopachagua, na huko mutawaendea makuhani wa Kilawi, na mwamuzi ambaye yuko katika kazi kwa wakati huo, nanyi mutatoa mashitaki kwao nao watawatangazia uamuzi wao. Kisha mutafanya kama vile watakavyowatangazia pale pahali Yawe atakapochagua. Mutakuwa waangalifu kufanya yote kama vile watakavyowaagiza. Itawapasa kufanya kufuatana na maongozi watakayowapatia na uamuzi watakaotoa kwenu. Musiache kutimiza hukumu watakayowatangazia kwa kupita kuume au kushoto. Naye mutu atakayetenda kwa kiburi bila kutii kuhani aliyewekwa hapo kwa kumutumikia Yawe, Mungu wenu, au mwamuzi, mutu huyo atauawa. Ndivyo mutakavyokomesha uovu kati yenu. Watu wote watasikia na kuogopa wasifanye tena kitu kwa kiburi. “Mutakapokwisha kuingia katika inchi ambayo Yawe, Mungu wenu, anawapa, mukirizi na kukaa humo, nanyi mukisema kwamba mutaweka mufalme juu yenu, kama vile mataifa yote yanayowazunguka, munaweza kumuweka mufalme juu yenu mutu ambaye Yawe, Mungu wenu, atamuchagua. Mutamuweka mumoja wa wandugu zenu kuwa mufalme juu yenu. Musimufanye mugeni asiyekuwa ndugu yenu kuwa mufalme wenu. Hata hivyo, asikuwe na farasi wengi kwa ajili yake mwenyewe, wala asiwarudishe watu Misri kwa kujipatia farasi zaidi, kwa sababu Yawe amewaonya: ‘Hamutarudi tena kwa njia ile.’ Wala asijipatie wake wengi; kama sivyo moyo wake utaasi. Wala asijipatie feza na zahabu kwa wingi sana. Atakapokuwa akiikalia kiti cha ufalme anapaswa kuandika mufano wa sheria hii katika kitabu kinachokuwa mbele ya makuhani wa Kilawi. Mufano huo atakuwa nao siku zote na kuusoma maisha yake yote, kusudi apate kujifunza kumwogopa Yawe, Mungu wake, akishika na kutimiza maneno yote ya sheria hii na masharti haya, bila kujitukuza mwenyewe juu ya wandugu zake, wala kuiweka kando amri hii kwa namna yoyote, kusudi aweze kudumu katika utawala, yeye na wazao wake katika Israeli. “Makuhani Walawi, ni kusema kabila lote la Lawi, wasikuwe na sehemu wala urizi katika Israeli. Wao watakula sehemu ya sadaka za Yawe. Wala wasikuwe na urizi kati ya wandugu zao; Yawe ndiye urizi wao kama vile alivyoahidi. “Na hii itakuwa haki ya makuhani kutoka kwa watu wanaotolea sadaka ikuwe ni ngombe au kondoo: watamupa kuhani muguu wa mbele, mashavu na matumbotumbo. Mutawapa sehemu ya kwanza ya mazao yenu ya ngano, divai, mafuta yenu na sufu ya kwanza ya kondoo wenu. Katika makabila yenu yote, Yawe amechagua kabila la Walawi limutumikie kama vile makuhani milele. “Ikiwa Mulawi yeyote atapenda mwenyewe anaweza kutoka katika muji wowote wa Israeli kwenda pale pahali Yawe alipochagua, na hapo anaweza kutumika kwa jina la Yawe, Mungu wake, kama wale Walawi wengine wanaotumika mbele ya Yawe. Watapata mafungu yao sawa ya kula, ingawa wako na mapato kutokana na kuuzisha mali za jamaa zao. “Mutakapofika katika ile inchi Yawe, Mungu wenu, anayowapa, musifuate zile tabia za kuchukiza za mataifa ya huko. Kusikuwe mutu yeyote kati yenu anayemupitisha kwenye moto mutoto wake mwanaume au mwanamuke kuwa tambiko, wala mutu anayepiga ramuli, wala mwaguzi, wala mwenye kufanya uganga, wala muchawi, wala mulozi, wala mwenye kutaka shauri kwa mizimu na pepo au kutoka kwa wafu. Maana yeyote anayetenda mambo haya ni chukizo kwa Yawe; na kwa ajili ya mambo haya ya kuchukiza Yawe, Mungu wenu, anafukuza watu wa namna hiyo mbele yenu. Mukuwe wakamilifu mbele ya Yawe, Mungu wenu. Kwa maana mataifa haya ambayo mutairizi inchi yao wanafuata maongozi ya waaguzi na wapiga ramuli; lakini Yawe, Mungu wenu hawaruhusu ninyi kufanya hivyo. “Yawe, Mungu wenu atawachagulia nabii anayekuwa kama mimi kutoka kati yenu wenyewe, nanyi mutamutii huyo. Hicho ndicho mulichomwomba Yawe, Mungu wenu, kule Horebu, siku ile mulipokusanyika na kusema: ‘Tusisikie tena sauti ya Yawe, Mungu wetu, wala tusiuone tena moto huu mukubwa, kusudi tusikufe!’ Naye Yawe akaniambia: ‘Wamesema ukweli. Nitawachagulia kati ya wandugu zao wenyewe nabii kama wewe, nitatia maneno yangu ndani ya kinywa chake, naye atawaambia yote nitakayomwamuru. Yeyote ambaye hatasikia maneno nabii huyo atakayosema kwa jina langu, mimi mwenyewe nitamwazibu. Lakini nabii yeyote atakayesema kwa jina la miungu mingine, au atakayejaribu kusema neno kwa jina langu wakati mimi sikumwambia aseme, huyo nabii atakufa.’ “Lakini ninyi munaweza kusema: ‘Tutaweza namna gani kutambua neno ambalo Yawe hakulisema?’ Kama nabii akisema kitu aseme ni kwa jina la Yawe, na kitu hicho hakifanyiki au hakiko kweli, jambo hilo Yawe hakulisema; nabii amelisema kwa kiburi, nanyi musitishwe na jambo hilo. “Wakati Yawe, Mungu wenu, atakapoteketeza watu wale ambao anawapa ninyi inchi yao, na kisha kuitwaa na kuishi katika nyumba zao, mutatenga miji mitatu katika inchi Yawe, Mungu wenu atakayowapatia muirizi. Mutatengeneza barabara na kugawanya katika sehemu tatu inchi ambayo Yawe, Mungu wenu, atawapatia muirizi kusudi yeyote anayemwua mutu bila kukusudia apate kukimbilia huko. “Mutu kwa bahati mbaya akimwua mwenzake bila kukusudia ambaye kwanza hakuwa adui yake, kwa mufano, mutu anayekwenda na mwenzake katika pori kukata kuni naye wakati anakata muti, shoka likachomoka kutoka kwenye mupini wake, na kumwua yule mwingine, mutu huyo anaweza kukimbilia kwenye muji mumoja, kwa kuokoa maisha yake. Lakini kama umbali wa muji huo ni mukubwa sana, huyo mwenye kulipiza kisasi, kwa hasira kali anaweza kumufuatilia, akimukamata na kumwua huyo aliyesababisha kifo, ingawa hakupewa hukumu ya kifo na hao wawili hawakukuwa waadui mbele. Kwa hiyo mimi ninawaamuru mutenge miji mitatu. “Tena kama vile Yawe, Mungu wenu, akipanua mipaka ya inchi yenu, kama vile alivyowaapia babu zenu, naye akiwapatia inchi yote ambayo aliahidi kuwapatia hao babu zenu ikiwa mutakuwa waangalifu kushika amri hizi zote, ninazowaamuru hivi leo, mukimupenda Yawe, Mungu wenu, na kufuata siku zote njia zake, basi, mutaongeza miji mingine mitatu zaidi ya hii mitatu, kusudi mutu asiyekuwa na kosa asiuawe katika inchi yenu ambayo Yawe, Mungu wenu, atawapatia kuwa yenu, na hivyo kuwasababisha kuwa na kosa la mauaji. “Lakini mutu akiwa adui wa mwenzake, akivizia, akimushambulia na kumwua, kisha anakimbilia kwenye muji mumoja wa miji hiyo, hapo wazee wa muji huo watatuma watu wamutoshe kule na kumutoa kwa mwenye kulipiza kisasi cha umwangaji wa damu, auawe. Musimwonee huruma, lakini mutakomesha uovu wa mauaji ya mutu asiyekuwa na kosa katika Israeli, kusudi mupate kuishi kwa amani. “Musiondoe kitambulisho cha mipaka ya wajirani zenu, ambayo iliwekwa hapo zamani katika inchi ambayo Yawe wenu anawapatia muirizi. “Ushuhuda wa mutu mumoja hautoshi kwa kuhukumu mutu juu ya kosa lolote au uovu juu ya kosa lolote alilofanya. Ni ushuhuda wa watu wawili au watatu tu ndio utakaohakishwa. Ikiwa mushuhuda wa uongo atatokea kwa kumushitaki mutu yeyote juu ya kosa fulani, basi hao wote wawili wanaobishana watakwenda mbele ya Yawe, mbele ya makuhani na waamuzi ambao wako katika kazi wakati huo. Waamuzi watachunguza kwa uangalifu maneno hayo na ikiwa mushuhuda ni mushuhuda wa uongo na amemushitaki mwenzake kwa uongo, basi, mutamutendea sawa vile alivyokusudia kumutendea ndugu yake. Ndivyo mutakavyokomesha uovu kati yenu. Nao watu wengine watasikia na kuogopa, na uovu kama huo hautafanyika tena kati yenu. Musiwaonee huruma watu wa aina hiyo. Uzima utalipwa kwa uzima, jicho kwa jicho, jino kwa jino, mukono kwa mukono na muguu kwa muguu. “Mukienda kwa vita kupigana na waadui zenu, mukiona farasi, magari na jeshi kubwa zaidi kuliko lenu musiwaogope. Maana Yawe, Mungu wenu, aliyewatoa Misri, atakuwa nanyi. Mbele ya kuanza mapigano, kuhani atajitokeza mbele na kuwaambia watu: ‘Watu wa Israeli musikilize! Leo munakaribia kupigana na waadui zenu. Musivunjike moyo, au kuogopa, au kutishwa, au kuwaogopa waadui; maana Yawe, Mungu wenu, ndiye atakayekwenda pamoja nanyi kupigana kwa ajili yenu mbele ya waadui zenu na kuwapa ushindi’. “Kisha wakubwa watawaambia watu: ‘Kuna mutu yeyote hapa aliyejenga nyumba mupya lakini hajaizindua? Arudie kwake, kusudi asikufie kwenye vita na mutu mwingine aizindue. Kuna mutu yeyote hapa aliyepanda mizabibu na ambaye hajafurahia matunda yake ya kwanza? Arudi kwake asikufie kwenye vita na mutu mwingine afurahie matunda yake. Kuna mwanaume yeyote hapa aliyechumbia na yuko karibu kuoa? Arudie kwake, kusudi asikufie kwenye vita, na mwanaume mwingine aoe muchumba wake. Kuna mutu aliyevunjika moyo? Arudie kwake, kusudi asiwavunje wenzake moyo kama vile yeye.’ Wakubwa wakisha kusema na watu, basi majemadari watawaongoza watu. “Munapokaribia muji kwa kuushambulia, kwanza muwape wakaaji wake masharti ya amani. Wakaaji wa muji huo wakitaka amani na kujitoa kwenu, basi watu wote wanaokuwa humo watawatumikia na kufanya kazi za kulazimishwa. Lakini wakaaji wa muji huo wasipofanya amani nanyi, lakini wakipigana vita nanyi, basi, mutazunguka muji wao kwa vita, naye Yawe, Mungu wenu, akiutia katika mikono yenu, mutawaua kwa upanga wanaume wote. Lakini wanawake na watoto, ngombe, na vyote vinavyokuwa katika muji, vitu vyake vyote munaweza kuvibeba kwa ajili yenu wenyewe. Munaweza kufurahia vitu vya waadui zenu, ambavyo Yawe, Mungu wenu, amewapa. Ndivyo mutakavyoitendea miji yote ambayo iko mbali na inchi mutakayorizi. Lakini katika miji ya inchi ambayo Yawe, Mungu wenu, anawapa, musiache kitu chochote. Mutawaangamiza watu wote: Wahiti, Waamori, Wakanana, Waperizi, Wahivi na Wayebusi kama vile Yawe, Mungu wenu alivyoamuru, kusudi wasiwafundishe desturi zao za kuchukiza ambazo wanafanyia miungu yao, nanyi mutende zambi mbele ya Yawe, Mungu wenu. “Munapozunguka muji kwa muda murefu, mukipigana vita na kuuteka, musiharibu miti ya matunda kwa mashoka. Miti ni watu hata ishambuliwe nanyi? Munaweza kula matunda ya miti hiyo, lakini musiikate. Munaweza kukata tu miti mingine kwa kuitumia kwa kujenga ngazi za kupandia ndani ya muji munaoshambulia mpaka uanguke. “Mutu akipatikana ameuawa katika mbuga katika inchi ambayo Yawe, Mungu wenu, anawapa kuwa urizi wenu, nanyi hamujui ni nani aliyemwua, wazee na waamuzi wenu watajitokeza na kupima umbali wa kutoka pahali maiti inapokuwa mpaka kwenye miji ya karibu. Kisha, wazee wa muji ule unaokuwa karibu zaidi na ile maiti watatwaa mwana-ngombe ambaye hajatumiwa kufanya kazi yoyote wala kutiwa nira. Nao watamuteremusha mwana-ngombe katika bonde kwenye kijito ambacho hakikauki, na bonde hilo halilimwi au kupandwa. Huko watamuvunja huyo mwana-ngombe shingo. Nao makuhani wa ukoo wa Lawi sharti wakuwe pale. Yawe, Mungu wenu, aliwachagua wamutumikie na kubariki kwa jina lake. Wao vilevile ndio wenye mamlaka ya kuamua magomvi na maneno juu ya kuumizana. Yule mwana-ngombe atakapovunjwa shingo, wazee wote wa muji huo unaokuwa karibu na mutu huyo aliyeuawa, watanawa mikono yao kwa maji juu ya mwana-ngombe na kusema: ‘Hatuna kosa juu ya kifo hiki, wala hatumujui aliyemwua. Ee Yawe, uwasamehe watu wako wa Israeli ambao umewakomboa, usiwawekee watu wako Israeli kosa la mauaji ya mutu asiyekuwa na kosa, lakini uwasamehe kosa lile.’ Hivyo damu hiyo iliyomwangwa haitakuwa tena sababu ya hukumu kwenu, maana mumefanya yale Yawe aliyotaka mufanye. “Mukienda kupigana vita na adui, naye Yawe akiwapa ushindi, na kuteka vitu, kama mumoja wenu akiona kati ya vitu vilivyotekwa mwanamuke muzuri, akimutamani na kutaka kumwoa, basi, anaweza kumupeleka kwake. Yule mwanamuke atanyoa kichwa chake na kukata kucha zake, na kubadilisha nguo zake za kitumwa. Atakaa muda wa mwezi muzima kwa kumwomboleza baba yake na mama yake. Kisha mwanaume huyo anaweza kumwoa. Kama kisha hapendezwi naye, atamwacha aende anakotaka. Mwanaume huyo hatamwuzisha kwa kupata feza, wala hatamutendea kama vile mutumwa kwa sababu amemunyenyekeza. “Ikiwa mwanaume fulani ana wake wawili naye anamupenda mumoja kuliko mwingine, nao wanawake hao wamemuzalia watoto wanaume, na mutoto wa kwanza kuzaliwa ni wa yule mama asiyemupenda, ikifika siku ya kuwapa hao wanawake urizi, huyo baba haruhusiwi kumutendea mutoto wa yule muke anayemupenda kama kwamba ni mutoto muzaliwa wa kwanza, pahali pa yule mutoto wa mama asiyependwa ambaye ndiye anayekuwa muzaliwa wa kwanza. Anapaswa kukubali yule muzaliwa wa kwanza, mutoto wa yule mwanamuke asiyependwa, na kumupa haki yake: sehemu ya mali zake mara mbili. “Kama mutu ana mutoto mwenye kiburi na mwasi, asiyemutii baba yake au mama yake ingawa wanamwazibu, basi, mama na baba ya huyo mutoto watamutwaa kumupeleka kwa wazee muji kwenye tribinali. Wazazi hao watawaambia wazee wa muji: ‘Mutoto wetu ni mwenye kiburi na mwasi, hataki kutusikiliza, ni mulafi na mulevi’. Hapo watu wa muji huo watamupiga mutoto huyo mawe mpaka akufe. Ndivyo mutakavyokomesha ubaya huo kati yenu. Kila mutu katika Israeli atasikia tukio hilo na kuogopa. “Kama mutu amefanya kosa linalomupasa auawe na akiuawa kwa kutundikwa juu ya muti, maiti yake isiachwe juu ya muti usiku wote, lakini mutaizika siku hiyohiyo. Maana mutu aliyetundikwa amelaaniwa na Mungu nanyi hamutachafua inchi yenu muliyopewa na Yawe, Mungu wenu, ikuwe urizi wenu. “Ukimwona ngombe au kondoo wa ndugu yako amepotea, usimwache, lakini umurudishe kwa ndugu yako. Lakini kama nyumba ya huyu ndugu si karibu au kama haumujui mwenyeji, basi, utatwaa nyama huyo kwako, akae kwako mpaka mwenyeji atakapokuja, nawe utamurudishia naye. Utafanya vivyo hivyo kwa punda au vazi au kitu chochote ambacho ndugu yako amekipoteza. Usiache kumusaidia. “Ukiona punda au ngombe wa ndugu yako ameanguka katika njia, usiache kumusaidia ndugu yako; utamusaidia kumwinua. “Wanawake wasivae nguo za wanaume, na wanaume wasivae nguo za wanawake. Anayefanya hivyo ni chukizo kwa Yawe, Mungu wenu. “Ukikuta chicha ya ndege juu ya muti au katika njia, inayokuwa na vitoto au mayai na mama ndege amefunika hivyo vitoto au mayai, usitwae mama ndege na vitoto vyake. Utamwacha mama ndege aende zake, lakini unaweza kutwaa vitoto. Ukifanya hivyo utafanikiwa na kuishi maisha marefu. “Unapojenga nyumba, jenga ukuta pembeni ya paa, kusudi usihukumiwe kama mutu akianguka kutoka huko, na kufa. “Usipande mizabibu yako pamoja na mimea mingine, kama sivyo mazao yote yatakuwa haramu, siyo tu yale uliyopanda lakini vilevile matunda ya mizabibu. “Usilime shamba kwa kutumia ngombe na punda pamoja. “Usivae nguo zilizofumwa kwa sufu na kitani. “Funga vishada katika pembe ine za nguo yako. “Kama mwanaume anamwoa mwanamuke, halafu kisha akakata shauri la kumwacha, na kumushitaki kwamba ametenda mambo ya haya, na kumuharibishia sifa yake kwa kusema kwamba hakukuwa bikira wakati alipomwoa, basi, kama ikitokea hivyo, wazazi wa huyo binti watapeleka ushuhuda wa ubikira wa binti yao kwa wazee kwenye mulango wa muji na kuwaambia: ‘Tulimwoesha binti yetu huyu kwa mutu huyu, lakini sasa hamutaki tena, na ajabu ni kwamba ameshitaki mambo ya haya na kusema kwamba hakumukuta na ushuhuda wowote kwamba alikuwa bikira. Hata hivyo ushuhuda wa ubikira wa binti yetu ni huu’. Halafu atakunjua nguo yenye huo ushuhuda mbele ya wazee wa muji. Hapo wazee wa muji watamupeleka yule mwanaume na kumwazibu. Vilevile watamulipisha mutu huyo malipo ya vikoroti mia moja vya feza na kupewa baba wa huyo mwanamuke kwa sababu mwanaume huyo amemuharibishia binti wa Israeli sifa. Na huyo mwanamuke ataendelea kuwa muke wake na hataweza kuachana naye maisha yake yote. Lakini kama mashitaki hayo ni ya kweli, na hakuna ushuhuda wa ubikira wake, watamupeleka kwenye mulango wa nyumba ya baba yake na wanaume wa muji huo watamupiga mawe akufe, kwa sababu amefanya upumbafu katika Israeli kwa kufanya ukahaba akiwa katika nyumba ya baba yake. Ndivyo mutakavyokomesha uovu huo kati yenu. “Mutu akikamatwa akilala na muke wa mutu mwingine, wote wawili, mwanaume na mwanamuke, wanapaswa kuuawa. Ndivyo mutakavyokomesha uovu huo kati yenu. “Mwanaume akimukuta binti aliyechumbiwa, akilala naye, mutawatoa wote wawili inje ya muji na kuwapiga mawe mpaka wakufe. Binti huyo anapaswa kuuawa kwa sababu hakupiga kelele kusudi asaidiwe ingawa alikuwa ndani ya muji; naye mwanaume anapaswa kuuawa kwa sababu amemuchafua muchumba wa mwenzake. Ndivyo mutakavyokomesha uovu huo kati yenu. “Lakini kama mwanaume amekutana na binti aliyechumbiwa akamushika kwa nguvu, basi ni huyo mwanaume tu atakayeuawa. Musimutendee huyo binti chochote; yeye hana kosa linalostahili azabu ya kifo. Tukio hili ni sawa na la mutu anayemushambulia mutu mwingine na kumwua, kwa sababu mwanaume huyo alimushika kwa nguvu huyo binti huko katika mbuga, na ingawa alipiga kelele kwa kuomba musaada hakukuwa mutu wa kumusaidia. “Mwanaume akikutana na binti ambaye hajachumbiwa, akimushika kwa nguvu, wakikamatwa, mwanaume huyo atamulipa baba wa binti huyo vikoroti makumi tano vya feza kwa sababu amemuchafua, na binti huyo atakuwa muke wake na hatamwacha maisha yake yote. “Mwanaume yeyote asilale na muke wa baba yake. “Mwanaume yeyote aliyeumizwa au aliyekatwa kiungo chake cha kiume haruhusiwi kujiunga na kusanyiko la watu wa Yawe. “Na mwana haramu yeyote, wala muzao wake hata kizazi cha kumi, haruhusiwi kuingia katika kusanyiko la watu wa Yawe. “Mwamori au Mumoabu yeyote, wazao wao wote hata kizazi cha kumi, hawaruhusiwi kuingia katika kusanyiko la watu wa Yawe, kwa sababu walikataa kuwapatia chakula na maji mulipokuwa katika njia kutoka Misri, na kwa sababu walimulipa Balamu mwana wa Beori kutoka Petori kule Mesopotamia, awalaani. Lakini Yawe, Mungu wenu, hakumusikiliza Balamu; pahali pake laana hiyo iligeuka kuwa baraka, kwa sababu Yawe, Mungu wenu, aliwapenda. Kwa hiyo, musiwasaidie hao hata kidogo kusudi wapate amani na fanaka. “Musiwachukie Waedomu; hao ni wandugu zenu. Na musiwachukie Wamisri, maana mulikaa katika inchi yao kama vile wageni. Wazao wao, kuanzia kizazi cha tatu, wataruhusiwa kuingia katika kusanyiko la watu wa Yawe. “Mukienda kwa vita, mukipiga kambi, kila mumoja afanye angalisho na kitu chochote kiovu. Kama kati yenu kuna mutu yeyote ambaye ni muchafu kwa sababu ya kutokwa mbegu usiku, huyo atatoka inje ya kambi; hatakaa karibu na kambi. Lakini ikifika magaribi ataoga, na jua likitua anaweza kurudi katika kambi. “Munapaswa kuwa na pahali inje ya kambi ambapo munaweza kwenda kwa choo. Kati ya vifaa vyenu mutakuwa na jembe, na hilo mutalitumia kuchimba shimo na kufukia mavi yenu. Kambi yenu inapaswa kuwa takatifu kwa sababu Yawe, Mungu wenu anatembea katika kambi yenu kusudi awaokoe na kuwatia waadui zenu katika mikono yenu. Kwa hiyo musimwache aone kitu chochote kisichofaa kati yenu, kama sivyo atawaacha ninyi. “Mutumwa akikimbilia kwako usimurudishe kwa bwana wake. Ataishi pamoja nawe pahali atakapochagua katika moja ya makao yako, pahali panapomupendeza. Usimutese. “Mwisraeli yeyote, mwanaume au mwanamuke, hatakuwa hata kidogo kahaba wa kidini. Feza yoyote iliyopatikana na vitendo vya ukahaba huo, isipelekwe ndani ya hekalu la Yawe, Mungu wenu, kwa kulipia kiapo, maana mwanaume au mwanamuke anayekuwa kahaba wa kidini ni chukizo kwa Yawe. “Usimukopeshe ndugu yako Mwisraeli kitu kwa faida; usimulipishe faida juu ya mukopo wa feza, chakula, au chochote ambacho watu wanakopesha kwa faida. Unaweza kuomba faida unapomukopesha mugeni, lakini ndugu yako Mwisraeli usimulipishe faida, naye Yawe, Mungu wako, atakubariki katika shuguli zako zote utakazofanya katika inchi ambayo unakwenda kurizi. Unapofanya kiapo mbele ya Yawe, Mungu wako, usichelewe kukitimiza, maana Yawe, Mungu wako, atakidai kwako, nawe utakuwa na kosa. Lakini ukiacha kufanya kiapo hautakuwa na zambi. Ukuwe mwangalifu kutimiza kiapo ulichosema kwa mudomo wako, maana ulimwahidi Yawe, Mungu wako, kwa mapenzi yako. “Ukipitia katika shamba la muzabibu la mwenzako unaweza kula zabibu kadiri unavyoweza, lakini usichume na kupeleka zabibu zozote katika kikapu chako. Ukipitia katika shamba la mwenzako lenye ngano unaweza kukwanyua masuke kwa mukono na kula, lakini usitwae kisu kwa kukata mazao yake. “Ikiwa mwanaume ameoa muke na kisha hapendezwi naye kwa sababu ameona kwake kitu kisichofaa, basi, huyo mwanaume akimwandikia barua ya kuachana, akimupa na kumufukuza kutoka katika nyumba yake, kisha huyo mwanamuke akiondoka, na kuolewa na mwanaume mwingine, kama huyo mume wa pili akimutwaa, akimwandikia barua ya kuachana, akimupa na kumufukuza toka katika nyumba yake, au kama huyo mume wake akikufa, basi, yule mume wa kwanza haruhusiwi tena kumutwaa huyo mwanamuke kuwa muke wake kwa sababu alikwisha kuchafuliwa. Kufanya hivyo ni chukizo kwa Yawe. “Mwanaume aliyetoka kuoa asiende kwa vita wala asipewe kazi yoyote ingine; aachwe huru kwa muda wa mwaka mumoja, kusudi akae kwake na kufurahi na muke wake. “Mutu yeyote asitwae jiwe la chini au la juu la kusagia kuwa rehani; kufanya hivyo ni kama kutwaa uzima wa mutu huyo. “Mutu yeyote akimwiba Mwisraeli mwenzake na kumufanya kuwa mutumwa wake au kumwuzisha katika utumwa, mutu huyo anapaswa kuuawa. Ndivyo mutakavyokomesha uovu kati yenu. “Kama mutu akishikwa na ukoma munapaswa kuwa waangalifu kufuata maagizo ya Walawi. Kama vile nilivyowaamuru ndivyo mutakavyofuata kwa uangalifu. Mukumbuke jinsi Yawe, Mungu wenu, alivyomutendea Miriamu mulipokuwa katika safari kutoka Misri. “Ukimukopesha mwenzako kitu chochote, usiingie kwake kutwaa rehani. Usimame inje na umwache yeye mwenyewe akuletee hiyo rehani. Kama yeye ni masikini usikae na rehani hiyo usiku kucha. Umurudishe kila siku magaribi kusudi usiku aweze kujifunika na kukutakia baraka. Kufanya hivyo ni jambo la uhaki mbele ya Yawe, Mungu wenu. “Usimutese mutumishi wako wa mushahara anayekuwa masikini na muhitaji, akuwe Mwisraeli au mumoja wa wageni wanaoishi katika miji yenu. Kila siku, mbele jua halijatua, umulipe mushahara wake wa siku hiyo, maana yeye ni masikini na huo mushahara ni tegemeo la moyo wake; kusudi asimulilie Yawe, nawe utakuwa na kosa. “Wazazi wasiuawe kwa makosa ya watoto wao, wala watoto wasiuawe kwa ajili ya makosa ya wazazi wao. Kila mutu atauawa kwa makosa yake mwenyewe. “Musipotoshe haki za wageni na wayatima. Wala musitwae nguo ya mujane kuwa rehani. Mukumbuke kwamba ninyi mulikuwa watumwa katika inchi ya Misri, na Yawe, Mungu wenu, akawakomboa kutoka huko. Kwa hiyo ninawapa amri hiyo. “Munapovuna mavuno yenu katika shamba na kusahau masuke mengine humo, musirudi kuyatwaa, lakini muwaachie wageni, wayatima na wajane, kusudi Yawe, Mungu wenu, awabariki katika kazi zenu zote. Munapotikisa mizeituni yenu kwa kuvuna matunda, musirudi kutikisa tena vitawi vyake, lakini muwaachie wageni, wayatima na wajane. Munapochuma zabibu, musirudi kuokota zabibu zilizobaki lakini muwaachie wageni, wayatima na wajane. Mutakumbuka kwamba ninyi mulikuwa watumwa katika inchi ya Misri; kwa hiyo ninawapa ninyi amri hii. “Ikiwa kuna ugomvi kati ya watu wawili, na wakienda kwa tribinali kuamua maneno yao, mumoja akionekana hana kosa, na mwingine akihukumiwa, kama yule aliyehukumiwa amepewa azabu ya kupigwa fimbo, mwamuzi atamwamuru huyo alale chini na kupigwa fimbo kulingana na kosa lake. Mwenye kosa anaweza kupigwa fimbo makumi ine lakini si zaidi. Mukizidisha kiasi hicho mutakuwa mumemufezehesha ndugu yenu. “Usimufunge ngombe kinywa anapopepeta ngano. “Kama wandugu wanaishi pahali fulani na mumoja wao akikufa bila kuacha mutoto mwanaume, muke wa marehemu asiolewe na mutu mwingine inje ya jamaa hiyo. Yule ndugu wa marehemu anapaswa kumwoa mujane huyo. Mutoto wa kwanza mwanaume atakayezaliwa nao atahesabiwa kuwa wa marehemu kusudi jina lake lisifutwe katika inchi ya Israeli. Lakini kama huyo ndugu wa marehemu hamutaki huyo mwanamuke mujane, basi, mwanamuke huyo atakwenda mbele ya wazee wa muji na kusema: ‘Kaka wa mume wangu marehemu anakataa kuendelesha jina la kaka yake marehemu katika Israeli; hapendi kunitimizia madaraka yake ya kaka wa mume wangu marehemu’. Kisha wazee wa muji watamwita huyo mwanaume na kuongea naye. Kama ataendelea kukataa kwamba hataki kumwoa, huyo mwanamuke mujane atamwendea mbele ya hao wazee wa muji, atamuvua kiatu chake kimoja na kumutemea mate kwenye uso na kumwambia: ‘Hivi ndivyo anavyopaswa kutendewa mutu anayekataa kudumisha nyumba ya kaka yake’. Na jina la nyumba yake katika Israeli litakuwa: ‘Nyumba ya mutu aliyevuliwa kiatu.’ ” “Wanaume wawili wakipigana na muke wa mumoja wao akimusaidia mume wake kwa kumukamata sehemu za siri yule anayepigana na mume wake, mutakata mukono wa kuume wa yule mwanamuke; musimuhurumie. “Musikuwe na vipimo vya kupimia vya namna mbili: kimoja kizito na kingine chepesi. Musitumie mizani za udanganyifu. Wala musikuwe na aina mbili za vipimo vya kupimia, kubwa na ndogo. “Mutumie mizani na vipimo vyenye uzito kamili na vya haki mupate kuishi maisha marefu katika inchi Yawe, Mungu wenu, anayowapa. Wote wanaofanya mambo hayo, wote wanaotenda kwa udanganyifu ni chukizo kwa Yawe, Mungu wenu. “Mukumbuke kitendo cha Waamaleki mulipokuwa katika safari kutoka Misri. Mukumbuke jinsi walivyowashambulia huko katika njia mukiwa wazaifu na kuwapiga wale wote waliokuja nyuma yenu wamechoka. Waamaleki hawakumwogopa Mungu. Kwa hiyo wakati Yawe, Mungu wenu, atakapowapumzisha kutokana na mashambulio ya waadui zenu wote wanaowazunguka katika inchi ambayo amewapa kuwa urizi wenu na kuishi humo, munapaswa kuangamiza Waamaleki wote. “Na kisha kufika na kurizi inchi ambayo Yawe, Mungu wenu anawapa ikuwe yenu na kuishi huko, utatwaa malimbuko ya mazao utakayovuna katika inchi Yawe, Mungu wenu, anayokupa, na kuyaweka katika kikapu mpaka pale pahali ambapo Yawe, Mungu wenu, amechagua pawe makao yake. Utamwendea kuhani anayetumika wakati huo, na kumwambia: ‘Leo ninashuhudia mbele ya Yawe, Mungu wangu, kwamba nimeingia katika inchi aliyowaapia wazee wetu kwamba atatupatia’. “Naye kuhani atakapotwaa kikapu hicho toka mikono yako na kukiweka mbele ya mazabahu ya Yawe, Mungu wako, utasema maneno haya mbele ya Yawe, Mungu wako: ‘Baba yangu alikuwa Musuria aliyetangatanga huko na huko, kisha akashuka kwenda Misri akaishi huko kama mugeni. Yeye na jamaa yake walikuwa watu wachache tu walipokuwa huko, lakini wakakuwa taifa kubwa lenye nguvu na watu wengi. Wamisri walitutendea kwa ukali wakatutesa na kutulazimisha kufanya kazi ngumu ya watumwa. Kisha tukamulilia Yawe, Mungu wa wazee wetu, akasikia kilio chetu, na kuona mateso yetu, kazi ngumu na mateso tulizozipata. Basi, Yawe akatutoa huko Misri kwa mukono wake wa nguvu ulionyooshwa, kwa vitisho, vitambulisho na maajabu. Akatuleta hapa na kutupatia inchi hii inayotiririka maziwa na asali. Na sasa ninamuletea Yawe malimbuko ya mazao ya inchi ambayo amenipa’. “Kisha utaweka kikapu chini, mbele ya Yawe, Mungu wako, na kuabudu mbele yake. Nawe utafurahia mema yote ambayo Yawe, Mungu wako, amekujalia wewe na jamaa yako. Nao watafurahi pamoja nawe. Kila nyuma ya miaka mitatu, kila mumoja wenu atatoa sehemu ya kumi ya mazao yake yote kwa ajili ya Walawi na wageni, wayatima na wajane, kusudi wapate chakula chote wanachohitaji wanapokuwa katika miji yenu. Kisha utasema mbele ya Yawe, Mungu wako, hivi: ‘Nimetoa katika nyumba yangu fungu takatifu, nikawapa Walawi, wageni, wayatima na wajane, kama vile ulivyoniamuru nifanye. Sijavunja amri zako wala sijasahau. Sikukula sehemu ya kumi yoyote nilipokuwa ninaomboleza; sikuitoa inje ya nyumba yangu nilipokuwa muchafu na sikutoa sehemu ya kumi hiyo kwa wafu. Nimekutii ee Yawe, Mungu wangu; nimefanya kila kitu ulichoamuru juu ya sehemu ya kumi. Uangalie chini kutoka makao yako matakatifu mbinguni, uwabariki watu wako Israeli na inchi uliyotupatia kama vile ulivyowaapia wazee wetu; inchi inayotiririka maziwa na asali’. “Leo hii, Yawe, Mungu wenu, anawaamuru kushika masharti na maagizo haya. Mukuwe waangalifu kuyatimiza kwa moyo wote na roho yote. Leo Yawe ameahidi kwamba atakuwa Mungu wenu, kama mutafuata njia zake na kushika masharti, amri, na maagizo yake na kutii sauti yake. Nanyi mumeahidi kwamba mutakuwa watu wake yeye mwenyewe na kwamba mutashika amri zake zote. Atawafanya ninyi kuwa taifa kubwa kuliko mataifa yote aliyoumba. Nanyi mutatetea jina lake, sifa yake na heshima yake. Ninyi mutakuwa watakatifu wake kama vile alivyosema.” Basi, Musa akiwa pamoja na wazee wa Israeli aliwaambia watu hivi: “Mushike amri zote ninazowapa leo. Siku ile mutakapovuka muto Yordani na kuingia katika inchi ambayo Yawe, Mungu wenu, amewapa, mutasimika mawe makubwa na kuyapiga lipu. Juu yake mutaandika maneno yote ya sheria hizi zote, mutakapoingia katika inchi ile inayotiririka maziwa na asali, ambayo Yawe, Mungu wa wazee wenu, aliwaahidi. Mukiwa ngambo ya muto Yordani, mutasimika mawe hata juu ya mulima Ebali, kama vile ninavyowaamuru hivi leo, na kuyapiga lipu. Mutamujengea Yawe, Mungu wenu, mazabahu pahali pale panapokuwa na mawe ambayo hayakuchongwa. Mutamujengea Yawe, Mungu wenu, mazabahu kwa mawe yasiyochongwa. Juu ya mazabahu hiyo mutamutolea Yawe, Mungu wenu, sadaka za kuteketezwa. Mutamutolea sadaka za amani, na kula hapohapo na kufurahi mbele ya Yawe, Mungu wenu. Mutaandika waziwazi juu ya mawe hayo maneno yote ya sheria hii.” Basi, Musa pamoja na makuhani Walawi wakawaambia watu wote wa Israeli: “Munyamaze munisikilize enyi watu wa Israeli. Leo hii ninyi mumekuwa watu wa Yawe, Mungu wenu. Kwa hiyo mutatii sauti ya Yawe, Mungu wenu, mukifuata amri zake na masharti yake ambayo ninawaamuru leo.” Siku hiyo Musa akawaagiza watu na kusema: “Mukisha kuvuka Yordani, makabila haya yatasimama juu na mulima Gerizimu kwa kubariki watu: Simeoni, Lawi, Yuda, Isakari, Yosefu na Benjamina. Na makabila haya yatasimama juu ya mulima Ebali wakati laana zitakapotolewa: Rubeni, Gadi, Aseri, Zebuluni, Dani na Nafutali. Nao Walawi watatangazia watu wote wa Israeli kwa sauti kubwa: “ ‘Alaaniwe mutu yeyote anayefanya sanamu ya kuchonga au ya kuyeyushwa na kuisimamisha kwa siri, kitu ambacho kimetengenezwa na mikono ya fundi na ambacho ni chukizo kwa Yawe, Mungu wenu’. Na watu wote wataitika: ‘Amina!’ “ ‘Alaaniwe mutu yeyote anayezarau baba yake au mama yake.’ Na watu wote wataitika: ‘Amina!’ “ ‘Alaaniwe mutu yeyote anayeondoa kitambulisho cha mupaka wa mwenzake.’ Na watu wote wataitika: ‘Amina!’ “ ‘Alaaniwe mutu yeyote anayemupotosha kipofu katika njia.’ Na watu wote wataitika: ‘Amina!’ “ ‘Alaaniwe mutu yeyote anayepotosha haki ya mugeni au yatima au mujane’. Na watu wote wataitika: ‘Amina!’ “ ‘Alaaniwe mwanaume anayelala na muke wa baba yake, maana amemupatisha baba yake haya’. Na watu wote wataitika: ‘Amina!’ “ ‘Alaaniwe mutu yeyote anayelala na nyama yoyote’. Na watu wote wataitika: ‘Amina!’ “ ‘Alaaniwe mutu yeyote anayelala na dada yake akuwe ni binti ya baba yake au binti ya mama yake’. Na watu wote wataitika: ‘Amina!’ “ ‘Alaaniwe mutu yeyote anayelala na mama mukwe wake’. Na watu wote wataitika: ‘Amina!’ “ ‘Alaaniwe mutu yeyote anayeua mutu kwa siri’. Na watu wote wataitika: ‘Amina!’ “ ‘Alaaniwe mutu yeyote anayepokea kituliro kusudi aue mutu asiyekuwa na kosa’. Na watu wote wataitika: ‘Amina!’ “ ‘Alaaniwe mutu yeyote asiyekubali maneno haya ya sheria na kuyatii’. Na watu wote wataitika: ‘Amina!’ “Kama mukiitii sauti ya Yawe, Mungu wenu, na kushika kwa uangalifu amri ambazo ninawaamuru leo, yeye atawaweka juu ya mataifa yote katika dunia. Kama mukitii sauti ya Yawe, Mungu wenu, mutapewa baraka hizi: “Miji yenu itabarikiwa na mashamba yenu. “Mutabarikiwa mupate wazao wengi, mavuno mengi, ngombe na kondoo wengi. “Vikapu vyenu vya ngano vitabarikiwa na vyombo vyenu vya kupondea mukate. Mutabarikiwa munaporudi kwa nyumba na munapotoka inje. Waadui zenu wakiwashambulia, Yawe atawapa ushindi juu yao. Wakikuja kuwashambulia kwa njia moja watawakimbia kwa njia saba. Baraka za Yawe zitakuwa katika gala zenu za ngano na katika shuguli zenu zote. Atawabariki katika inchi ambayo anawapa. “Yawe atawafanya kuwa watu wake watakatifu kama vile alivyowaahidi, kama mukitii amri zake yeye Yawe, Mungu wenu, na kufuata njia zake. Mataifa yote katika dunia yakiona kwamba ninyi munaitwa kwa jina la Yawe yatawaogopa. Yawe atawafanikisha kwa wingi: watoto, mifugo na mavuno katika shamba katika inchi aliyowaapia wazee wenu kwamba atawapa. Yawe atawafungulia hazina yake nzuri kutoka mbinguni na kunyesha mvua katika inchi kwa wakati wake, na kubariki kazi zenu. Mutakopesha mataifa mengi, lakini ninyi hamutakopa. Yawe, Mungu wenu, atawafanya kuwa wa kwanza kwa nguvu na sio wa mwisho. Mutaendelea mbele na sio kurudi nyuma kama mukishika amri zake ambazo ninawapa leo na kuwa waangalifu kwa kuzitimiza, bila kugeuka kuume au kushoto kwa kufuata miungu mingine na kuitumikia. “Lakini kama hamutaitii sauti ya Yawe, Mungu wenu, kama hamutakuwa waangalifu kushika amri zake zote na masharti ninayowaamuru leo, basi mutapatwa na laana hizi zote: Mutapata laana katika miji yenu na mashamba yenu. Vikapu vyenu vya ngano vitalaaniwa na vyombo vyenu vya kupondea mukate. Watoto wenu watalaaniwa na mazao yenu ya inchi; mifugo yenu italaaniwa isiongezeke. Mutalaaniwa munapoingia na munapotoka. “Yawe atawatumia laana, mashaka na kukata tamaa katika shuguli zenu zote mpaka muangamie upesi kwa sababu ya uovu wa matendo yenu na kwa sababu ya kumwacha Yawe. Atawaletea ugonjwa mukali mpaka ninyi wote muangamie kabisa katika inchi ambayo munaenda kurizi. Yawe atawashambulia kwa kifua kikuu, homa, majipu, joto kali, ukavu, zoruba na ukungu; mambo hayo yatawaandama mpaka muangamie. Mbingu zitakauka kama shaba nyeusi bila mvua, na inchi itakuwa kama chuma. Yawe ataifanya vumbi na muchanga kuwa mvua yenu, vumbi itawanyeshea mpaka muangamie. “Yawe atawafanya mushindwe na waadui zenu. Ninyi mutakwenda kuwashambulia kwa njia moja, lakini mutawakimbia kwa njia saba. Nanyi mutakuwa kinyaa kwa watu wote katika dunia. Maiti zenu zitakuwa chakula cha ndege wala hakutakuwa mutu atakayewafukuza. Yawe atawapiga kwa majipu yaliyowapata Wamisri, atawapa vidonda, upele na kuwashwa ambavyo hamuwezi kuponywa. Yawe atawapiga kwa pigo la kuwa na wazimu, mutakuwa vipofu na kuvurugika akili. Mutakwenda kwa kupapasapapasa muchana kama vipofu wala hamutafanikiwa katika shuguli zenu. Mutakuwa munateswa kila mara na hakutakuwa mutu wa kuwasaidia. “Mutachumbia wabinti lakini watu wengine watalala nao. Mukijenga nyumba watu wengine watakaa ndani yake. Mukipanda mizabibu watu wengine watavuna. Ngombe wenu watachinjwa mbele ya macho yenu lakini hamutaonja hata kipande cha nyama yao. Punda wenu watatwaliwa kwa nguvu mbele ya macho yenu wala hamutarudishiwa. Kondoo wenu watapewa waadui zenu, na hakuna mutu atakayeweza kuwasaidia. Watoto wenu wanaume na wanawake watatolewa kwa watu wengine nanyi mutakodoa macho muchana kutwa kuwatazamia warudi, lakini hamutakuwa na nguvu ya kufanya chochote. “Taifa musilolijua litatwaa mazao yote ya inchi yenu na matunda ya jasho lenu, nanyi mutapondwa na kuteswa siku zote, hata mutapata wazimu kwa mambo mutakayoona kwa macho yenu wenyewe. Yawe atashambulia magoti yenu na miguu yenu kwa majipu makali ambayo hamutaweza kuponywa; yatawaenea tangu juu ya kichwa mpaka kwenye vikanyagio vya miguu. “Yawe atawapeleka ninyi na mufalme wenu mutakayejichagulia, mpaka kwa taifa ambalo ninyi hamukulijua wala wazee wenu. Na huko mutatumikia miungu mingine ya miti na mawe. Nanyi mutakuwa kinyaa, mazarau na mushangao kati ya watu wote wa inchi ambako Yawe atawapeleka. Mutapanda mbegu nyingi lakini mutavuna kidogo tu kwa sababu nzige watakula mazao yenu. Mutapanda mizabibu na kuitunza, lakini hamutavuna mizabibu hiyo wala kunywa divai yake, maana wadudu wataikula. Mutakuwa na mizeituni pahali pote katika inchi yenu, lakini hamutakuwa na mafuta ya kujipakaa, kwa sababu zeituni hizo zitaangukaanguka. Mutazaa watoto wanaume na wanawake, lakini hawatakuwa wenu, watapelekwa katika uhamisho. Matunda yenu yote na mazao yenu katika mashamba vitashambuliwa na nzige. “Wageni wanaoishi katika inchi yenu watazidi kupata nguvu wakati ninyi mutazidi kufifia zaidi na zaidi. Wao watawakopesha ninyi, lakini ninyi hamutakuwa na uwezo wa kuwakopesha. Wao watakuwa wa kwanza kwa nguvu nanyi mutakuwa wa mwisho. “Hayo yote yatawapata ninyi na kuwaandama mpaka muangamie kwa sababu hamukutii sauti ya Yawe, Mungu wenu, juu ya kushika amri zake na masharti aliyowapa. Lakini hizo zitakuwa ushuhuda wa hukumu ya Yawe kwenu na wazao wenu milele. “Yawe, Mungu wenu aliwabariki katika kila njia, lakini ninyi hamukumutumikia kwa moyo wa furaha na shangwe. Kwa hiyo mutawatumikia waadui zenu ambao Yawe atawatuma mbele yenu, kwa njaa, kiu na uchi, na ukosefu wa kila kitu. Atawafunga nira ya chuma mpaka awaangamize. “Yawe ataleta kutoka mbali taifa moja liwashambulie mbio kama tai, taifa ambalo hamujui luga yake. Watu wa taifa hilo watakuwa na nyuso kali. Hawatajali wazee wala kuwahurumia vijana. Watakula ngombe wenu na mazao yenu, mpaka muangamie. Hawatawaachia ngano, divai, mafuta, ngombe au kondoo mpaka wawaangamize. Watu hao watawazunguka katika miji yenu yote, mpaka kuta zenu za makimbilio ambazo mulitegemea zimeporomoshwa chini kila pahali katika inchi yenu ambayo Yawe, Mungu wenu, amewapa. Wakati wa kuzungukwa na kutaabishwa na waadui zenu, mutakula watoto wenu ambao Yawe, Mungu wenu, amewapa. Hata mutu mupole kabisa na aliyelelewa vizuri sana hatafurahi kuona ndugu yake, muke wake aliyemupenda na mutoto wake atakayebakia, wala hatamugawanyia hata mumoja wao nyama ya watoto wake atakaowakula. Hamutabakiliwa na chochote wakati huo wa kuzungukwa na kutaabishwa na waadui katika miji yenu yote. Hata mwanamuke yule ambaye ni mupole sana na aliyelelewa vizuri na mwenye kupendeza ambaye hajasubutu kukanyaga udongo kwa kikanyagio chake, hatafurahi kuona mume wake aliyemupenda na watoto wake. Wakati huo wa kuzungukwa kutakuwa njaa hata atakula mutoto wake muchanga kwa siri nyuma ya kumuzaa pamoja na nyama ya kizazi kwa sababu ya ukosefu wa chakula. “Kama musipokuwa waangalifu kwa kushika maneno yote ya sheria hii iliyoandikwa katika kitabu hiki na musipoheshimu na kutukuza jina tukufu la kuogopesha la Yawe, Mungu wenu basi, Yawe atawaletea ninyi na wazao wenu mateso yasiyokuwa ya kawaida, mateso makali yasiyoponyeshwa na ya kudumu, na magonjwa makali ya kudumu. Atawaletea tena yale magonjwa muliyoyaogopa katika inchi ya Misri, nayo yatawaandama siku zote. Atawaletea magonjwa ya kila aina na mateso mengine ambayo hayakutajwa katika kitabu hiki cha sheria mpaka muangamie. Ijapokuwa ninyi ni wengi kama nyota za mbinguni, lakini mutakuwa wachache tu kwa sababu hamukutii sauti ya Yawe, Mungu wenu. Kama vile Yawe alivyopendezwa kuwafanikisha na kuwafanya kuwa wengi, ni vile vile Yawe atapendezwa kuwaletea hasara na kuwaangamiza. Nanyi mutaondolewa katika inchi hiyo ambayo munakwenda kuirizi. Yawe atawatawanya kati ya mataifa yote, kutoka pembe moja ya dunia mpaka nyingine na huko mutaitumikia miungu mingine ya miti na mawe, miungu ambayo ninyi wala wazee wenu hamukuijua. Hamutakuwa na raha yoyote pahali penu wenyewe pa kutulia wala kati ya mataifa hayo. Lakini Yawe atawapa huko wasiwasi wa moyo, kufifia kwa macho na mahangaiko ya ndani ya roho. “Maisha yenu yatakuwa katika mashaka, muchana na usiku mutakuwa na hofu na hamutakuwa na usalama wa maisha. Mioyo yenu itajaa woga wa kila kitu mutakachoona. Asubui mutasema ‘Heri ingekuwa magaribi’; magaribi itakapofika mutasema ‘Heri ingekuwa asubui’. Yawe atawarudisha Misri kwa mashua, safari ambayo aliahidi kwamba hamungeifanya tena. Huko mutajaribu kujiuzisha kwa waadui zenu kuwa watumwa, lakini hakuna mutu atakayewanunua.” Haya ni maneno ya agano ambalo Yawe aliwaamuru Musa kufanya na Waisraeli katika inchi ya Moabu, zaidi ya agano Yawe alilofanya nao kwenye mulima Horebu. Musa akawaita pamoja Waisraeli wote akawaambia: “Muliona ninyi wenyewe jinsi Yawe alivyomutendea mufalme wa Misri, wakubwa, watumishi wake na inchi yake yote. Muliona majaribu makubwa, vitambulisho na maajabu aliyotenda. Lakini mpaka leo Yawe hajawapa ninyi akili ya kuelewa, macho ya kuona, wala masikio ya kusikia! “Kwa muda wa miaka makumi ine, mimi niliwaongoza katika jangwa, nguo zenu mulizovaa hazikuchakaa wala viatu vyenu havikuchakaa kwenye miguu yenu. Hamukukula mukate wala kunywa divai au kileo chochote. Na hivyo mutapata kujua kwamba Yawe ni Mungu wenu. “Na mulipofika pahali hapa, mufalme Sihoni wa Hesiboni na mufalme Ogi wa Basani walikuja kupigana nasi; lakini tukawashinda, tukakamata inchi yao, tukayagawanyia makabila ya Rubeni na Gadi na nusu kabila la Manase ikuwe mali yao. Kwa hiyo mukuwe waangalifu kushika maneno yote ya agano hili kusudi mupate kufanikiwa katika kazi zenu zote. “Leo, mumesimama mbele ya Yawe, Mungu wenu, ninyi wote viongozi wa makabila, wazee wenu, wakubwa wenu, watoto wenu na wake zenu, wageni wanaoishi kati yenu ambao wanakata kuni na kuwatekea maji. Muko hapa leo kwa kufanya agano pamoja na Yawe, Mungu wenu na kulihakikisha kwa kiapo. Kwa hiyo leo mutakuwa watu wake naye atakuwa Mungu wenu, kama vile alivyowaapia ninyi na babu zenu Abrahamu, Isaka na Yakobo. Wala sifanyi agano hili leo kwa ajili yenu tu na kutamka laana zake; sifanyi kwa ajili ya wale tu wanaokuwa pamoja nasi leo mbele ya Yawe, Mungu wetu lakini vilevile kwa ajili ya wale ambao hawapo pamoja nasi leo. “Munajua jinsi tulivyoishi katika inchi ya Misri na jinsi tulivyosafiri katika inchi za mataifa mengine. Muliona sanamu zao za kuchukiza, miungu ya miti na mawe, ya feza na zahabu. Mufanye angalisho kwamba hakuna mwanaume, mwanamuke, jamaa au kabila lolote linalosimama hapa leo litakalomwacha Yawe, Mungu wetu, kwenda kutumikia miungu ya mataifa mengine. Jambo hili litakuwa kama muzizi utakaoota na kuzaa matunda machungu yenye sumu. Kisha kusikia maneno ya agano hili ambayo mumeapishwa, na mutu akijiamini mwenyewe ndani ya moyo wake na kusema atakuwa salama naye akifuata ugumu wake, hiyo italeta maangamizi. Yawe hatasamehe mutu huyo, nayo hasira ya Yawe na wivu wake vitamuwakia mutu huyo. Laana zote zilizoandikwa katika kitabu hiki zitamupata, naye Yawe atafuta kabisa jina la mutu huyo kutoka katika dunia. Yawe atamutenga kutoka kati ya makabila yote ya Israeli apatwe na hasara kufuatana na laana zote za agano zilizoandikwa katika kitabu hiki. Katika vizazi vinavyokuja, wazao wenu na wageni kutoka inchi ya mbali wataona jinsi Yawe alivyoletea inchi hii hasara na mateso. Wataona kwamba imejaa kiberiti na chumvi, imechomwa na kuwa tupu, haikupandwa mbegu na haioti chochote. Ni kama vile ilivyokuwa wakati Yawe alipoangamiza Sodoma na Gomora, Adima na Seboimu, kwa hasira yake kali. Hata mataifa yote yatasema: ‘Kwa nini Yawe ameitendea hivyo inchi hii? Hasira hii kubwa ina maana gani?’ Na jibu hili litatolewa: ‘Ni kwa sababu walivunja agano la Yawe, Mungu wa wazee wao ambalo alifanya nao alipowatoa katika inchi ya Misri. Wakaenda kutumikia na kuabudu miungu mingine, ambayo hawakuijua mbele, wala Yawe hakukuwa amewapa. Kwa hiyo hasira ya Yawe ikawaka juu ya inchi hii, na kuiletea laana zote zilizoandikwa katika kitabu hiki. Naye Yawe, akawaongoza kutoka katika inchi yao kwa hasira na kasirani kubwa, akawatupa katika inchi nyingine kama vile inavyokuwa leo’. “Mambo ya siri ni ya Yawe, Mungu wetu, lakini yale ambayo ameyafunua ni yetu na wazao wetu milele, kusudi tushike maneno yote ya sheria hii.” Musa akaendelea kusema: “Baraka na laana hizi zote zitatimizwa. Mutafikiri juu ya mambo hayo wakati Yawe, Mungu wenu, atakuwa amewatawanya kati ya mataifa. Mukimurudilia Yawe, Mungu wenu, ninyi na watoto wenu, mukitii kwa moyo wote na roho yote neno lake ninalowaamuru leo, hapo Yawe, Mungu wenu, atawarudishia mema yenu na kuwahurumia na kuwakusanya tena kutoka katika mataifa ambamo atakuwa amewatawanya. Na hata kama mumetawanywa katika sehemu mbali kabisa katika dunia, Yawe, Mungu wenu, atawakusanya na kuwarudisha, kwa kurizi tena inchi ambamo wazee wenu waliishi. Naye atawafanya mufanikiwe zaidi na kuwa wengi kuliko wazee wenu. Yawe, Mungu wenu, atawafanya ninyi na wazao wenu mukuwe na moyo wa utii kusudi mumupende yeye kwa moyo wenu wote na roho yenu, mupate kuishi. Yawe, Mungu wenu, atafanya laana hizi zote ziwapate waadui zenu ambao waliwatesa. Nanyi mutatii sauti ya Yawe na kushika amri zake zote ninazowapa leo. Yawe, Mungu wenu, atawafanya mufanikiwe katika kila mutakalofanya; mutakuwa na watoto wengi na ngombe wengi na mashamba yenu yatatoa mazao. Maana atapenda tena kuwafanya mufanikiwe kama vile alivyopenda kuwafanikisha wazee wenu, ikiwa mutatii sauti yake na kushika amri na masharti yake yaliyoandikwa katika kitabu hiki cha sheria na kumurudilia Yawe, Mungu wenu, kwa moyo wote na roho yote. “Amri ninazowapa leo si ngumu sana kwenu, wala haziko mbali nanyi. Haziko mbinguni hata museme: ‘Nani atakayepanda juu mbinguni kutuletea kusudi tupate kuzisikia na kuzitii?’ Wala haziko ngambo ya bahari, hata museme: ‘Nani atakayevuka bahari atuletee kusudi tuzisikie na kuzitii.’ Sivyo, lakini neno hili liko karibu nanyi, ndani ya vinywa vyenu na ndani ya mioyo yenu, mupate kulitimiza. “Leo hii ninawapa uchaguzi kati ya mema na mabaya, kati ya uzima na kifo. Kama mukitii amri za Yawe, Mungu wenu, ambazo ninawapa leo, mukimupenda Yawe, Mungu wenu, na kufuata njia zake na kushika amri, masharti na maagizo yake, basi, mutaishi na kuongezeka; naye Yawe, Mungu wenu, atawabariki katika inchi ambayo munakwenda kuirizi. Lakini mukipotoshwa na kukataa kumusikiliza, mukivutwa kuabudu miungu mingine na kuitumikia, mimi ninawatangazia leo hii kwamba mutaangamia. Hamutaishi kwa muda murefu katika inchi munayokwenda kurizi, ngambo ya muto Yordani. Ninaita mbingu na inchi zishuhudie juu yenu leo hii, kwamba nimewapa uchaguzi kati ya uzima na kifo, kati ya baraka na laana. Basi, muchague uzima ninyi na wazao wenu mupate kuishi. Mumupende Yawe, Mungu wenu. Muitii sauti yake na kuambatana naye. Kama munafanya hivyo, mutapata maisha marefu na kuishi katika inchi ambayo Yawe aliwaahidi wazee wenu, Abrahamu, Isaka na Yakobo, kwamba atawapa.” Musa akaendelea kusema na Waisraeli wote, akawaambia: “Mimi sasa nina umri wa miaka mia moja na makumi mbili, na sina nguvu ya kufanya kazi zaidi. Tena Yawe ameniambia kwamba sitavuka muto Yordani. Yawe, Mungu wenu, atawatangulia na kuyaangamiza mataifa yanayoishi huko, kusudi murizi inchi yao. Yoshua atakuwa kiongozi wenu kama vile Yawe alivyosema. Yawe atayaangamiza mataifa hayo kama vile alivyowaangamiza Sihoni na Ogi, wafalme wa Waamori, na inchi yao. Yawe atawapa ushindi juu yao nanyi mutawatendea kama vile nilivyowaamuru. Mukuwe imara na hodari, wala musiwaogope au kutishwa nao, maana Yawe, Mungu wenu, ndiye anayekwenda pamoja nanyi. Yeye hataacha kuwasaidia na hatawatupa.” Kisha Musa akamwita Yoshua, akamwambia mbele ya watu wote wa Israeli: “Ukuwe imara na hodari, maana wewe utawaongoza watu hawa kwenda kurizi inchi ambayo Yawe aliwaahidi babu zao, nawe utawapatia wairizi. Yawe ndiye anayewaongoza. Yeye atakuwa pamoja nanyi. Yeye hataacha kuwasaidia na hatawatupa. Hivyo, musiogope wala musifazaike.” Basi, Musa akaandika sheria hiyo, akawapa makuhani wa ukoo wa Lawi ambao walikuwa wakibeba Sanduku la Agano la Yawe, na wazee wote wa Israeli. Kisha akawaamuru akasema: “Kila mwaka wa saba utakuwa mwaka wa mafungulio. Katika sikukuu ya vibanda, mwaka huo, wakati watu wa Israeli wanapokuja mbele ya Yawe pahali pale atakapochagua, mutawasomea watu wote wa Israeli sheria hii. Mutakusanya wanaume, wanawake, watoto na wageni wanaoishi katika miji yenu, kusudi kila mumoja asikie maneno haya ya kujifunza kumwogopa Yawe, Mungu wenu, na kuwa waangalifu kushika maneno ya sheria hii. Nao wazao wao ambao hawajasikia sheria ya Yawe, Mungu wenu, wapate kuisikia na kujifunza kumwogopa Yawe, Mungu wenu, muda wote mutakaoishi katika inchi ambayo munakwenda kurizi ngambo ya muto Yordani.” Yawe akamwambia Musa: “Siku yako ya kuaga dunia imekaribia. Umwite Yoshua, mukuje pamoja katika hema la mukutano kusudi nimupe maagizo.” Basi, Musa na Yoshua wakaenda katika hema la mukutano, naye Yawe akawatokea humo katika nguzo ya wingu ambayo ilisimama kwenye mulango wa hema. Yawe akamwambia Musa: “Umekaribia sasa kuaga dunia, na kisha kufa kwako, watu wataanza kuniacha na kuendea miungu mingine ya inchi hiyo ambamo watakwenda kuishi. Wataniacha na kuvunja agano nililoagana nao. Hapo hasira yangu itawawakia siku hiyo, nami nitawaacha na kuficha uso wangu mbali nao, wataangamizwa. Maovu mengi na taabu zitawapata hata watambue kwamba maovu hayo yamewapata kwa sababu Mungu wao hayuko kati yao. Hakika nitawaficha uso wangu kwa sababu wamefanya mambo maovu na kugeukia miungu mingine. “Sasa, andika wimbo huu, uwafundishe watu wa Israeli kusudi ukuwe ushuhuda wangu juu yao. Nitakapowapeleka katika inchi inayotiririka maziwa na asali, kama vile nilivyowaapia babu zao, nao watakula, watashiba na kunenepa, halafu watageukia miungu mingine na kuitumikia. Watanizarau na kuvunja agano langu. Watakapopatwa na hasara nyingi na taabu, wimbo huu utakuwa kama ushuhuda maana hautasahauliwa na wazao wao. Hata sasa, mbele sijawapeleka katika inchi niliyoapa kuwapa, ninajua mipango ambayo wanapanga.” Basi, Musa akaandika wimbo huo siku hiyohiyo, akawafundisha Waisraeli. Kisha Yawe akamwagiza Yoshua, mwana wa Nuni, akamwambia: “Ukuwe imara na hodari, maana utawaongoza Waisraeli katika inchi ambayo nimewaapia kuwapa, nami nitakuwa pamoja nawe.” Musa alipomaliza kuandika maneno ya sheria hiyo tangu mwanzo mpaka mwisho, akawaambia Walawi waliokuwa wanabeba lile Sanduku la Agano la Yawe: “Mutwae kitabu hiki cha sheria, mukiweke karibu na Sanduku la Agano la Yawe, Mungu wenu, kusudi kikuwe ushuhuda juu yenu. Maana ninajua jinsi munavyokuwa waasi na wagumu. Ikiwa mumemwasi Yawe wakati niko muzima pamoja nanyi, itakuwa namna gani nyuma ya kifo changu? Uwakusanye mbele yangu wazee wote wa makabila yenu na wakubwa wenu nipate kusema maneno haya wasikie, nayo dunia ishuhudie juu yao. Maana ninajua kwamba nyuma ya kifo changu hakika mutakuwa waovu na kuacha ile njia niliyowaamuru muifuate. Na katika siku zinazokuja mutapatwa na hasara kwa sababu mutafanya maovu mbele ya Yawe na kumukasirikisha kwa matendo yenu.” Halafu, Musa akasema maneno ya wimbo huu mbele ya kusanyiko lote la Waisraeli. Utege sikio, ee mbingu. Sikiliza, ee dunia, maneno ninayosema. Mafundisho yangu yatone kama mvua, maneno yangu yadondoke kama umande, kama manyunyu kwenye mimea michanga, kama mvua nyepesi katika majani mabichi. Maana nitatangaza jina la Yawe, nanyi museme: “Mungu wetu ni Mukubwa”. Yawe ni mulima wa usalama. Kazi zake ni kamilifu, njia zake zote ni za haki. Yeye ni Mungu mwaminifu asiyekuwa na kosa, yeye anafanya mambo ya usawa na ya haki. Lakini ninyi mumekosa uaminifu kwake, ninyi sio watoto wake tena kwa sababu ya uovu, ninyi ni kizazi kiovu na kipotovu. Munaweza namna gani kumulipa hivyo Yawe, enyi watu wapumbafu na wasiokuwa na akili? Yeye siye baba yenu aliyewaumba, aliyewafanya na kuwaimarisha? Mukumbuke siku zilizopita, mufikiri miaka ya vizazi vingi. Muulize baba zenu nao watawajulisha, muulize wakubwa wenu nao watawaelezea. Mungu Mukubwa alipogawanyia mataifa mali yao, alipowagawanyia wanadamu, kila taifa alilipatia mipaka yake, kulingana na hesabu ya wamalaika, lakini alijiwekea watu wa Yakobo kuwa wake, hao alijichagulia kuwa mali yake. Yawe alikuta Waisraeli katika inchi ya jangwa, jangwa tupu zenye upepo mukali. Aliwalinda na kuwatunza. Aliwakinga kama mboni ya jicho lake. Alikuwa kama tai anayelinda chicha yake, anayeruka karibu ya vitoto vyake, akitandaza mabawa yake kwa kuwashikilia, na kuwabeba juu ya mabawa yake. Yeye Yawe mwenyewe aliwaongoza na hakukuwa mungu mwingine wa kumusaidia. Aliwapitisha katika inchi za juu za vilima, nao wakakula mazao ya mashamba. Akawapa asali kutoka katika mawe waonje na mafuta kutoka katika jiwe gumu. Aliwapa siagi na maziwa ya mifugo, mafuta ya wana-kondoo na kondoo dume, makundi ya mifugo ya Basani na mbuzi. Aliwapa ngano nzuri kabisa na divai mupya wakakunywa. Watu wa usawa walinona, wakapiga mateke. Walinenepa sana, kisha wakamwacha Mungu aliyewaumba, wakazarau Mulima wa wokovu wao. Wakamufanya aone wivu mukali kwa miungu yao, wakamuchochea akasirike kwa matendo yao ya kuchukiza. Wakatambikia pepo ambazo hazikukuwa miungu, wakaendea miungu ambayo hawakuijua hata kidogo, miungu mipya iliyotokea kwa siku za karibu, ambayo wazee wao hawakuiheshimu hata kidogo. Hamukumujali Mulima wenu, yule aliyewapa uzima. Mulimusahau Mungu aliyewazaa ninyi. Yawe aliona jambo hilo akawaacha; aliwakataa watoto wake, wanaume na wanawake. Akasema hivi: Nitawaficha uso wangu nione mwisho wao utakuwa namna gani. Maana wao ni kizazi kipotovu, watoto wasiokuwa na uaminifu wowote. Wamenichochea kuona wivu kwa kitu kisichokuwa mungu, wamenikasirikisha kwa sanamu zao. Hivyo nitawafanya waone wivu juu ya watu wa bure, nitawakasirikisha kwa kutumia taifa la wapumbafu. Hasira yangu imewaka moto, inachoma mpaka chini kuzimu, itateketeza dunia na vinavyokuwa ndani yake, itaunguza misingi ya milima. Nitalundika hasara nyingi juu yao, nitawamalizia mishale yangu. Watakonda kwa njaa, wataangamizwa kwa homa kali. Nitaleta nyama wenye meno makali kuwashambulia, na nyoka wenye sumu wanaotambaa juu ya mavumbi. Vita itasababisha vifo vingi inje, na ndani ya nyumba hofu itawatawala. Vijana wanaume na wanawake watauawa, hata wenye kunyonya na wazee wenye imvi. Ningaliwaangamiza kabisa na kuwafanya wasikumbukwe tena na mutu yeyote, isipokuwa tu kwa sababu ya majivuno ya waadui zao, kusudi waadui zao wasifikiri kwamba wamepata kuwaangamiza, nami Yawe sikufanya kitu katika mambo haya! Israeli ni taifa lisilokuwa na akili, watu wake hawana ufahamu ndani yao. Wangekuwa na hekima wangejua kwa nini walishindwa, wangeweza kuelewa mwisho wao utakuwa namna gani. Mutu mumoja anaweza namna gani kuwashinda watu elfu moja, au watu wawili wanaweza namna gani kuwashinda watu elfu kumi, isipokuwa kama mulinzi wao amewatupa, Yawe amewaacha? Hata waadui zetu wenyewe wanajua wazi, mulinzi wao hana nguvu kama mulinzi wetu. Maana mizabibu yao ni mizabibu ya Sodoma, zimetoka katika mashamba ya Gomora. Zabibu zake ni zabibu zenye sumu, vishada vyake ni vichungu. Divai yao ni kama sumu ya nyoka, ina sumu kali ya nyoka kubwa. Sina njia ya kuwaazibu? Silaha zangu ziko katika mukono wangu. Ni kazi yangu kulipiza kisasi, mimi nitalipiza, wakati miguu yao itakapoteleza; maana siku yao ya hasara imefika mwisho wao uko karibu sana. Yawe atawatetea watu wake, na kuwahurumia watumishi wake, wakati atakapoona nguvu zao zimeisha wala hakuna aliyebaki, mufungwa au mutu huru. Ndipo Yawe atakapouliza watu wake: Iko wapi ile miungu yenu, mulinzi muliyekimbilia usalama? Iko wapi hiyo miungu iliyokula matoleo yenu na kunywa divai na sadaka zenu za kinywaji? Basi isimame, iwasaidie; muache hiyo ikuwe ulinzi wenu sasa! Muone kwamba mimi ni Mungu na wala hakuna mwingine isipokuwa mimi. Mimi ninaua na kuweka uzima, ninaumiza na kuponya, na hakuna anayeweza kumwokoa yeyote toka katika mikono yangu. Ninanyoosha mukono wangu mbinguni na kuapa: Kama vile ninavyoishi milele, nitanoa upanga wangu unaometemeta, nitanyoosha mukono kutoa hukumu, nitawalipiza kisasi waadui zangu, nitawaazibu wale wanaonichukia. Mishale yangu nitailewesha kwa damu, upanga wangu utashiba nyama, utalowana na damu ya vidonda na wafungwa na waadui wenye nywele ndefu. Enyi mataifa, mushangilie watu wake, maana yeye analipiza kisasi damu ya watumishi wake, anawalipiza kisasi wapinzani wake, na kuitakasa inchi ya watu wake. Musa alikuja mbele ya Yoshua, mwana wa Nuni, wakarudilia maneno ya wimbo huu, kusudi Waisraeli wote wausikie. Musa alipomaliza kuwaambia watu wa Israeli maneno haya yote, akawaambia: “Muweke ndani ya mioyo yenu maneno yote ambayo ninawapa leo. Muwaamuru watoto wenu kusudi wafuate kwa uaminifu maneno yote ya sheria hii. Maana sheria hii si maneno matupu lakini ni uzima wenu; kwa njia ya sheria hii, mutaishi maisha marefu katika inchi munayokwenda kurizi, ngambo ya muto Yordani.” Siku hiyohiyo, Yawe akamwambia Musa: “Panda juu ya mulima huu wa Abarimu, mulima Nebo katika inchi ya Moabu, kuelekea muji wa Yeriko, uiangalie inchi ya Kanana ninayowapa Waisraeli wairizi. Kulekule juu ya mulima utakufa na kukutana na wazee wako kama vile kaka yako Haruni alivyokufa katika mulima Hori na kukutana nao, kwa sababu ninyi wote wawili mulivunja uaminifu wenu kwangu mbele ya Waisraeli mulipokuwa kwenye maji ya Meriba, karibu na muji wa Kadesi, katika jangwa la Sini. Mukakosa kuhakikisha utakatifu wangu kati ya Waisraeli. Utaona inchi inayokuwa mbele yako, lakini hautaingia katika inchi hiyo ninayowapa Waisraeli.” Hii ndiyo baraka ambayo Musa, mutu wa Mungu aliwatakia Waisraeli mbele ya kufa kwake. Alisema hivi: Yawe alikuja kutoka mulima Sinai, alitutokea kutoka mulima Seiri, aliangaza kutoka mulima Parani. Alitokea kati ya maelfu ya wamalaika, na moto unaowaka katika mukono wake wa kuume. Yawe anawapenda watu wake, anawalinda watakatifu wake wote. Wanamufuata na kupata maagizo kutoka kwake. Musa alituamuru tutii sheria; ni mali ya taifa letu. Yawe akakuwa mufalme wa Israeli, wakati viongozi wao walipokutana, na makabila yote yalipokusanyika. Musa akasema juu ya kabila la Rubeni: “Rubeni aishi wala asikufe, na watu wake wasikuwe wachache.” Juu ya kabila la Yuda akasema: “Ee Yawe usikilize kilio cha kabila la Yuda; umurudishe tena kwa wandugu zake. Upigane kwa mikono yako kwa ajili yake, usaidie kabila la Yuda mbele ya waadui zake.” Juu ya kabila la Lawi, akasema: “Ee Yawe, upatie wazao wa Lawi shauri lako, shauri lako kwa hao waaminifu wako, ambao uliwajaribu huko Masa. Ulishindana nao kwenye maji ya Meriba. Walawi waliacha wazazi wao, wakawasahau wandugu zao, hawakuwatambua hata watoto wao, maana walifuata amri zako, na kushika agano lako. Na watafundisha wazao wa Yakobo maagizo yako; watafundisha watu wa Israeli sheria yako. Walawi watafukiza ubani mbele yako, sadaka nzima za kuteketezwa juu ya mazabahu yako. Ee Yawe, ubariki nguvu zao, ukubali kazi za mikono yao, uvunje nguvu za waadui zao, nguvu za wanaowachukia hata wasiinuke tena.” Juu ya kabila la Benjamina akasema: “Hili ni kabila Yawe analopenda, nalo linakaa salama karibu naye. Yeye analinda muchana kutwa, na kukaa kati ya milima yake.” Juu ya kabila la Yosefu akasema: “Yawe abariki inchi yake, kwa baraka nzuri kabisa kutoka juu, ibarikiwe kwa matunda bora yanaoiva kwa jua, kwa matunda ya kila mwezi, kwa mazao bora ya milima ya kale, na mazao tele ya milima ya kale. Inchi yake ijae yote yanayokuwa mazuri, ibarikiwe kwa huruma wa Yawe, ambaye alitokea katika kichaka. Baraka hizi zishukie watu wa kabila la Yosefu, aliyekuwa mukubwa kati ya wandugu zake. Utukufu wake ni utukufu wa ngombe dume wa kwanza, pembe zake ni za mbogo dume. Atazitumia kusukuma mataifa; yote atayasukuma mpaka miisho ya dunia. Efuraimu atakuwa na pembe hizo elfu kumi na Manase kwa maelfu.” Juu ya kabila la Zebuluni akasema: “Zebuluni na Isakari mufanikiwe katika shuguli zenu na munapokuwa katika mahema yenu. Watawaalika wageni kwenye milima yao, na huko watu watatolea sadaka. Maana wao watapata utajiri wao kutoka katika bahari na hazina zao katika muchanga wa pembeni ya bahari.” Juu ya kabila la Gadi, akasema: “Atukuzwe Mungu anayemupatia Gadi sehemu kubwa. Gadi anaikaa kama simba akwanyue mukono na mufupa wa kichwa. Alijichagulia eneo zuri kuliko yote, pahali sehemu ya kiongozi ilipotengwa. Aliwaongoza watu na kumutii Yawe, alitimiza mupango wa Mungu kwa Israeli.” Juu ya kabila la Dani akasema hivi: “Dani ni mwana-simba anayeruka kutoka Basani.” Juu ya kabila la Nafutali akasema: “Ee Nafutali uliyeshibishwa upendeleo, uliyejaa baraka za Yawe, inchi yako ni mpaka kwenye ziwa Kinereti na upande wake wa kusini.” Juu ya kabila la Aseri akasema: “Aseri abarikiwe kuliko watoto wote wa Yakobo, na upendelewe na wandugu zako wote; na achovye muguu wake katika mafuta. Miji yako itakuwa ya chuma na shaba. Usalama wako utadumu maisha yako yote!” Musa akamalizia kwa kusema: “Ee Israeli, hakuna anayekuwa kama Mungu wako, yeye anayeruka toka mbinguni kuja kukusaidia, anapita juu katika anga katika utukufu wake. Mungu wa milele ndiye kimbilio lenu; nguvu yake inaonekana katika dunia. Aliwafukuza waadui mbele yenu; aliwaamuru: ‘Muwaangamize.’ Kwa hiyo, watu wa Israeli wakakaa salama, wazao wa Yakobo peke yao, katika inchi iliyojaa ngano na divai, inchi ambayo anga lake linadondosha umande. Heri yenu ninyi Waisraeli. Nani anayekuwa kama ninyi, watu muliookolewa na Yawe, ambaye ndiye ngao ya musaada wenu, na upanga unaowaletea ushindi! Waadui zenu watakuja wananyenyekea mbele yenu, nanyi mutawakanyaga chini.” Basi, Musa akaondoka kwenye bonde la Moabu, akaenda kwenye mulima Nebo, akapanda juu ya kilele cha Pisiga kinachoelekeana na Yeriko. Hapo Yawe akamwonyesha inchi yote: toka Gileadi mpaka Dani, eneo lote la Nafutali, eneo la Efuraimu na Manase, eneo lote la Yuda mpaka bahari ya Mediteranea, jangwa la Negebu na eneo la jangwa la bonde la Yeriko, muji wa miti ya ngazi mpaka Soari. Kisha Yawe akamwambia Musa: “Hii ndiyo inchi ile niliyomwapia Abrahamu, Isaka na Yakobo kwamba nitawapa wazao wao. Nimekuonyesha uione kwa macho yako mwenyewe, lakini hautafika huko.” Basi, Musa mutumishi wa Yawe akakufa kule katika inchi ya Moabu kulingana na neno Yawe alilosema. Alizikwa katika bonde la Moabu, kuelekea muji wa Beti-Peori; lakini mpaka leo, hakuna mutu anayejua pahali alipozikwa. Musa alikuwa na umri wa miaka mia moja na makumi mbili alipokufa. Macho yake yalikuwa hayajafifia, na nguvu za mwili wake hazikupunguka. Waisraeli wakaomboleza kifo chake kwa muda wa siku makumi tatu kwenye inchi ya bonde la Moabu. Kisha siku za kilio na maombolezo ya kifo chake zikaisha. Yoshua mwana wa Nuni akajaa roho ya hekima, kwa sababu Musa alikuwa amemuwekea mikono yake. Hivyo Waisraeli wakamutii Yoshua na kufuata amri ambazo Yawe alimupa Musa. Hakujatokea tena nabii katika Israeli kama Musa, ambaye Yawe alisema naye uso kwa uso. Hakuna nabii mwingine ambaye alifanya vitambulisho na miujiza kama ile ambayo Yawe aliyomutuma Musa afanye mbele ya mufalme wa Misri, wakubwa wake na inchi yake yote. Hakuna nabii mwingine ambaye amefanya mambo makubwa na ya kutisha kama vile Musa alivyofanya mbele ya Waisraeli wote. Nyuma ya kifo cha Musa mutumishi wa Yawe, Yawe alimwambia Yoshua mwana wa Nuni, musaidizi wa Musa: “Mutumishi wangu Musa amekufa, sasa muvuke muto Yordani, wewe pamoja na Waisraeli wote mpaka kwenye inchi ile ambayo ninawapa. Kila pahali mutakapokanyaga nimewapa ninyi nafasi ile kama nilivyomwahidi Musa. Mipaka ya inchi yenu itakuwa hivi: upande wa kusini ni jangwa, kaskazini ni milima ya Lebanoni, mashariki ni muto ule mukubwa Furati, kupitia inchi yote ya Wahiti mpaka bahari ya Mediteranea upande wa magaribi. Hakuna mutu atakayekushinda siku zote za maisha yako. Nitakuwa pamoja nawe kama nilivyokuwa pamoja na Musa. Siku zote nitakuwa nawe wala sitakuacha hata kidogo. Ukuwe imara na hodari kwa sababu wewe utawaongoza watu hawa kuirizi inchi ambayo niliwaahidi kwamba nitawapa wazee wao. Ukuwe tu imara na hodari. Ukuwe mwangalifu na kushika sheria yote mutumishi wangu Musa aliyokuamuru. Fuata kila sehemu ya sheria hiyo nawe utafanikiwa popote utakapoenda. Hakikisha kwamba hautakisahau hata kidogo kitabu hiki cha sheria; lakini kila siku utajifunza kitabu hiki, muchana na usiku, kusudi upate kutimiza yote yaliyoandikwa humu, nawe utastawi na kufanikiwa. Kumbuka kwamba mimi nimekuamuru ukuwe imara na hodari. Usiogope wala usifazaike kwa sababu mimi Yawe, Mungu wako, niko pamoja nawe popote utakapoenda.” Kisha Yoshua akawaamuru viongozi wa watu: “Mupite katika kambi na kuwaamuru watu watayarishe chakula, kwa sababu kisha siku tatu mutavuka muto Yordani, kwenda kuirizi inchi ambayo Yawe, Mungu wenu, anawapa ikuwe mali yenu.” Yoshua akawaambia watu wa kabila la Rubeni na Gadi na nusu ya kabila la Manase: “Mukumbuke lile jambo ambalo Musa, mutumishi wa Yawe, aliwaamuru akisema: ‘Yawe, Mungu wenu, atawapa pahali pa kupumzika, na atawapa inchi hii’. Wake zenu, watoto wenu na nyama wenu wa kufugwa watabaki katika inchi hiyo ambayo Musa aliwapa, ngambo ya muto Yordani. Lakini wanaume wote hodari wakiwa na silaha watavuka muto na kuwatangulia wandugu zenu. Mutawasaidia mpaka Yawe atakapowapa wandugu zenu vilevile pahali pa kupumzika, kama vile alivyowapa ninyi, nao vilevile warizi inchi ambayo wanapewa na Yawe, Mungu wenu. Kisha mutarudi katika inchi ambayo ni mali yenu na kuirizi, inchi ambayo mulipewa na Musa, mutumishi wa Yawe, ngambo ya muto Yordani.” Wakamujibu Yoshua: “Mambo yote uliyotuamuru tutayafanya, na popote utakapotutuma tutakwenda. Kama vile tulivyomutii Musa katika mambo yote, ndivyo tutakavyokutii wewe; Yawe, Mungu wako, akuwe pamoja nawe kama alivyokuwa pamoja na Musa. Mutu yeyote atakayeasi amri yako au kukataa kutii maneno yako au jambo lolote unalomwamuru, atauawa. Lakini, wewe ukuwe na nguvu na kuwa hodari.” Basi, Yoshua mwana wa Nuni, akawatuma watu wawili kwa siri kutoka Sitimu waende kufanya upelelezi katika inchi ile na hasa muji wa Yeriko. Wakaenda, wakafika kwenye nyumba ya kahaba mumoja aliyeitwa Rahabu wakalala humo. Mufalme wa muji wa Yeriko akaambiwa: “Wanaume wawili Waisraeli wameingia katika muji leo usiku kwa kuipeleleza inchi.” Mufalme wa Yeriko akatuma watu kwa Rahabu, akisema: “Uwatoshe inje watu waliokuja katika nyumba yako maana wamekuja kuipeleleza inchi yote.” Lakini, yule mwanamuke alikuwa amekwisha kuwaficha watu hao wawili. Basi, akawaambia wajumbe hao: “Ni kweli kwamba hao watu walikuja kwangu, lakini mimi sikujua wametoka wapi. Wakati wa kufunga mulango wa muji giza lilipoingia, hao watu waliondoka. Kule walikokwenda mimi sijui; muwafuate upesi nanyi mutawapata.” Lakini Rahabu alikuwa amewapandisha hao wapelelezi juu ya dari na kuwaficha kwa vijiti vya kitani alivyokuwa ametandaza juu ya dari. Basi, wale watu waliotumwa na mufalme wakawafuatilia kwa kupitia njia iliyokuwa imeelekea kwenye vivuko vya Yordani. Na mara tu walipoondoka katika muji, mulango wa muji ukafungwa. Rahabu akawaendea hao wapelelezi juu kwenye dari mbele hawajalala, akawaambia: “Mimi ninajua kwamba Yawe amewapa inchi hii; tumepatwa na hofu juu yenu na wakaaji wote wa inchi hii wanatetemeka kwa sababu yenu. Maana tumesikia jinsi Yawe alivyoyakausha maji ya bahari Nyekundu mbele yenu mulipotoka inchi ya Misri, na jinsi mulivyowatendea wafalme wawili wa Waamori waliokuwa ngambo ya muto Yordani, ni kusema Sihoni na Ogi, ambao muliwaangamiza kabisa. Mara tu tuliposikia mambo hayo, tukavunjika moyo kabisa kwa sababu yenu, tukaishiwa nguvu kabisa. Yawe, Mungu wenu, ndiye Mungu juu mbinguni na chini katika dunia! Kwa hiyo basi, tafazali muniapie kwa jina la Yawe kwamba mutanitendea mema mimi na jamaa yangu kama vile mimi nilivyowatendea mema, na munipe uhakikisho kamili. Muahidi kwamba mutamwacha baba yangu na mama yangu, kaka zangu na dada zangu, na jamaa yao yote; hamutakubali tuuawe!” Wale watu wakamujibu: “Uzima wenu ni uzima wetu! Kama hamutaifichua siri yetu, Yawe atakapotupa inchi hii, tutakutendea kwa wema na uaminifu.” Basi, Rahabu akawashusha hao watu kwa kamba kupitia katika dirisha: nyumba yake ilikuwa imejengwa ikiambatana na ukuta wa muji wa Yeriko. Akawaambia: “Mwende kwenye mulima kusudi wale wanaowafuatilia wasiwakamate. Mujifiche kule kwa muda wa siku tatu, mpaka wale wanaowafuatilia watakapokuwa wamerudi katika muji. Kisha mutaweza kujiendea.” Hao watu wakamwambia: “Sisi tutalitimiza kabisa jambo ulilotufanyia tunaahidi kwa kiapo. Tutakapokuja katika inchi hii, funga kamba hii nyekundu kwenye dirisha ambalo umetuteremushia. Uwakusanye hapa kwako baba yako, mama yako na kaka zako na jamaa yote ya baba yako. Lakini mutu yeyote akitoka inje ya nyumba yako na kwenda katika njia atabeba lazima ya kifo chake yeye mwenyewe. Lakini kama mutu yeyote atakayekuwa ndani ya nyumba yako akiguswa tu, basi lazima ya kifo chake itakuwa juu yetu. Lakini kama ukimwambia mutu yeyote juu ya shuguli hii yetu, basi, sisi hatutatimiza kiapo ulichotuomba tukuapie.” Naye akawaambia: “Ikuwe jinsi mulivyosema.” Kisha akawaruhusu waende zao, nao wakaondoka. Naye akaifunga ile kamba nyekundu kwenye dirisha. Wapelelezi hao waliondoka wakaenda kwenye milima. Walikaa kule kwa muda wa siku tatu mpaka wale waliokuwa wanawafuatilia waliporudi katika muji Yeriko, nyuma ya kuwatafuta na kukosa kuwaona. Basi, hao wapelelezi wawili wakashuka kutoka kwenye milima, wakavuka muto na kumwendea Yoshua mwana wa Nuni. Wakamwambia yote yaliyowapata. Wakamwambia: “Hakika Yawe ameitia inchi yote katika mikono yetu. Tena wakaaji wa inchi hiyo wametetemeka kwa sababu yetu.” Asubui mapema Yoshua pamoja na watu wote wa Israeli walianza safari kutoka Sitimu. Walipofika kwa muto Yordani, walipiga kambi hapo kwa muda mbele ya kuvuka. Nyuma ya siku tatu, viongozi walipita katikati ya kambi hiyo, wakawaambia watu: “Mutakapoliona Sanduku la Agano la Yawe, Mungu wenu, limebebwa na makuhani Walawi, mutaondoka na kulifuata; ndivyo mutakavyojua njia ya kupita maana hamujapita huku hata kidogo. Lakini musilikaribie sana Sanduku la Agano; mukuwe kwa umbali wa kilometre moja hivi.” Yoshua akawaambia watu: “Mujitakase kwa sababu kesho Yawe atatenda maajabu kati yenu.” Kisha akawaambia makuhani: “Mutwae Sanduku la Agano, mutangulie nalo mbele ya watu.” Nao wakalitwaa na kutangulia mbele ya watu. Yawe akamwambia Yoshua: “Leo hii, nitaanza kukutukuza mbele ya watu wote wa Israeli kusudi wajue kwamba, kama vile nilivyokuwa pamoja na Musa, ndivyo vilevile nitakavyokuwa pamoja nawe. Utawaamuru hao makuhani wanaobeba Sanduku la Agano wasimame karibu na ukingo wa muto Yordani wakati watakapofika kule.” Kisha Yoshua akawaambia Waisraeli: “Musogee karibu mupate kusikia maneno ya Yawe, Mungu wenu.” Yoshua akaendelea kusema: “Sasa mutajulishwa kabisa kwamba Mungu Mwenye Uzima yuko kati yenu na kwamba atawafukuza mbele yenu Wakanana, Wahiti, Wahivi, Waperizi, Wagirgasi na Waamoni, na Wayebusi. Muangalie, Sanduku la Agano la Bwana wa dunia yote liko karibu kupita mbele yenu kuelekea muto Yordani. Sasa, muchague watu kumi na wawili kutoka makabila ya Israeli, kila kabila mutu mumoja. Wakati miguu ya makuhani wanaobeba Sanduku la Agano la Yawe, Bwana wa dunia yote, itakapoingia katika maji ya muto Yordani, maji ya muto huo yataacha kutiririka. Na yale yatakayokuwa yanatiririka kutoka upande wa juu yatajikusanya pamoja kama lundo.” Basi, watu waliondoka katika kambi zao kwa kwenda kuvuka muto Yordani, nao makuhani wakiwa wamebeba Sanduku la Agano walitangulia watu. Na mara tu hao waliobeba Sanduku la Agano walipofika Yordani na miguu yao ilipokanyaga kwenye ukingo wa muto ule (muto Yordani unafurika wakati wa mavuno), maji yaliyokuwa yanatiririka kutoka upande wa juu yalisimama na kulundikana mpaka kule Adamu kijiji kinachokuwa karibu na muji wa Zaretani. Maji yaliyokuwa yanateremuka kwenda katika bahari ya Araba, ni kusema bahari ya Chumvi, yalitoweka kabisa, watu wakavuka mbele ya Yeriko. Wakati Waisraeli walipokuwa wanavuka, makuhani waliokuwa wanalibeba Sanduku la Agano walisimama pahali pakavu katikati ya muto Yordani mpaka taifa lote likavuka. Taifa zima lilipokwisha kuvuka muto Yordani, Yawe akamwambia Yoshua: “Chagua watu kumi na wawili kati ya hao Waisraeli, ni kusema mutu mumoja kutoka kila kabila, uwaagize hivi: ‘Mutwae mawe kumi na mawili kutoka hapa katikati ya muto Yordani, kutoka hapa miguu ya makuhani ilipokuwa, mutwae mawe hayo, muyaweke pahali pale ambapo mutalala leo hii.’ ” Yoshua akawaita hao watu kumi na wawili ambao alikuwa amewachagua kati ya Waisraeli, kila kabila mutu mumoja, akawaambia: “Mulitangulie Sanduku la Agano la Yawe, Mungu wenu, mpaka katikati ya muto Yordani. Kila mumoja wenu abebe jiwe kwenye bega lake, jiwe moja kwa ajili ya kila kabila la Israeli. Jambo hilo litakuwa kitambulisho kati yenu; na watoto wenu watakapowauliza kwa siku zinazokuja: ‘Mawe haya yana maana gani kwenu?’ Ninyi mutawaambia: ‘Sanduku la Agano la Yawe lilipopitishwa katika muto Yordani, maji ya muto huo yalizuiliwa yasitiririke!’ Kwa hiyo mawe haya yatakuwa ukumbusho kwa Waisraeli milele.” Wale wanaume wakafanya kama vile walivyoamriwa na Yoshua, wakatwaa mawe kumi na mawili kutoka katikati ya muto Yordani, jiwe moja kwa ajili ya kila kabila la Israeli, kama Yawe alivyomwambia Yoshua, wakaenda nayo mpaka pahali pale walipolala, wakayaweka kule. Yoshua akasimika vilevile mawe kumi na mawili katikati ya muto Yordani, pahali pale miguu ya makuhani waliobeba lile Sanduku la Agano iliposimama. Mawe hayo yako kule mpaka hivi leo. Wale makuhani waliobeba Sanduku la Agano, walisimama katikati ya muto Yordani mpaka watu walipomaliza kutimiza kila kitu ambacho Yawe alimwamuru Yoshua awaambie watu; Yoshua alifanya yote ambayo Musa alikuwa amemwamuru. Watu wakaharakisha kuvuka muto, na watu wote walipokwisha kuvuka, wale makuhani wakawatangulia na lile Sanduku la Agano la Yawe. Wanaume wa kabila la Rubeni na la Gadi na nusu ya kabila la Manase waliwatangulia Waisraeli wakiwa na silaha zao, kama vile walivyoagizwa na Musa. Watu yapata elfu makumi ine wakiwa na silaha tayari kwa vita walipita mbele ya Yawe wakielekea bonde la muji wa Yeriko. Katika siku hiyo Yawe akamutukuza Yoshua mbele ya Waisraeli wote, nao wakamuheshimu Yoshua maisha yake yote kama walivyomuheshimu Musa katika maisha yake. Kisha Yawe akamwambia Yoshua: “Uamuru makuhani wanaobeba sanduku la agano, watoke katika muto Yordani.” Basi, Yoshua akawaamuru wale makuhani: “Mutoke katika muto Yordani.” Hao makuhani waliokuwa wanabeba lile Sanduku la Agano la Yawe walipotoka katikati ya muto Yordani, na kukanyaga ukingo wa muto, maji ya muto Yordani yakaanza kutiririka tena, na kufurika kama mbele. Waisraeli walivuka muto Yordani katika siku ya kumi ya mwezi wa kwanza, wakapiga kambi kule katika muji wa Gilgali, upande wa mashariki wa Yeriko. Yoshua akayasimika yale mawe kumi na mawili ambayo waliyatwaa kutoka muto Yordani, kule Gilgali. Kisha Yoshua akawaambia Waisraeli: “Watoto wenu watakapowauliza kwa siku zinazokuja: ‘Mawe haya yana maana gani?’ Mutawaambia hivi: ‘Taifa la Israeli lilivuka muto huu wa Yordani pahali pakavu.’ Mutawaambia kwamba Yawe, Mungu wenu, aliyakausha maji ya muto Yordani kwa ajili yenu mpaka mukavuka, kama vile alivyofanya kwa bahari Nyekundu. Akaikausha mbele yetu mpaka tulipovuka kusudi watu wote wa dunia wajue kwamba mukono wa Yawe una nguvu; nanyi mupate kumwogopa Yawe, Mungu wenu, milele.” Wafalme wote wa Waamori walioishi ngambo ya magaribi ya Yordani, na wafalme wote wa Wakanana waliokuwa kandokando ya bahari ya Mediteranea, waliposikia kwamba Yawe aliyakausha maji ya muto Yordani kwa ajili ya Waisraeli mpaka walipokwisha kuvuka, wakavunjika moyo; wakaishiwa nguvu kabisa kwa kuwaogopa Waisraeli. Wakati ule, Yawe akamwambia Yoshua: “Tengeneza visu vya jiwe gumu kusudi uwatahiri Waisraeli.” Basi, Yoshua akatengeneza visu hivyo vya jiwe gumu na kuwatahiri Waisraeli kule Gibea-Haraloti. Sababu ya kuwatahiri Waisraeli ni hii: Waisraeli wote, wanaume, waliotoka Misri ambao walikuwa na umri wa kwenda kwa vita, wote walikufa katika safari ndani ya jangwa nyuma ya kutoka katika inchi ya Misri. Hao wote waliotoka Misri walikuwa wametahiriwa, lakini wale wote waliozaliwa katika safari kule katika jangwa kisha kutoka Misri, walikuwa bado hawajatahiriwa. Waisraeli walisafiri kwa muda wa miaka makumi ine katika jangwa hata wanaume wote waliokuwa na umri wa kwenda kwa vita wakaangamia kwa kuwa hawakusikiliza mambo Yawe aliyosema. Yawe alikuwa amewaapia watu hao kwamba hawataiona inchi ile inayotiririka maziwa na asali ambayo yeye aliwaapia baba zao kwamba atawapa. Kwa hiyo ilikuwa watoto wa watu hao ambao Yawe aliowakomalisha kwa pahali pao. Na ni hao ndio Yoshua aliowatahiri, maana hawakukuwa wanatahiriwa wakati ule walipokuwa katika safari ndani ya jangwa. Wanaume wote walipokwisha kutahiriwa walikaa katika kambi mpaka walipopona. Kisha Yawe akamwambia Yoshua: “Leo hii nimewaondolea ile haya ya Misri.” Hivyo pahali pale pakaitwa Gilgali mpaka hivi leo. Waisraeli walipokuwa wamepiga kambi kule Gilgali wakafanya sikukuu ya Pasaka magaribi ya siku ya kumi na ine ya mwezi katika mabonde ya Yeriko. Kesho yake, ni kusema nyuma ya Pasaka, walikula mikate isiyotiwa chachu na mbegu zenye kukaangwa kutokana na mazao ya inchi ile. Basi, tangu siku hiyo walipokula mazao ya inchi hiyo, Waisraeli hawakupata mana tena. Tangu mwaka ule Waisraeli walikula mazao ya inchi ya Kanana. Siku moja Yoshua alipokuwa karibu na muji wa Yeriko, aliona kwa rafla mutu mumoja akisimama mbele yake na upanga uliochomolewa katika mukono wake. Yoshua akamwendea, akamwuliza: “Wewe ni wetu au ni wa waadui zetu?” Naye akamujibu: “Wala wenu wala wa waadui zenu! Lakini mimi ni jemadari wa jeshi la Yawe, na sasa nimefika.” Yoshua akainama chini kwa heshima, kisha akamwuliza: “Bwana wangu, unataka mimi mutumishi wako nifanye nini?” Huyo jemadari wa jeshi la Yawe akamwambia: “Vua viatu vyako kwa maana pahali unaposimama ni patakatifu.” Yoshua akafanya hivyo. Milango ya kuingilia katika muji wa Yeriko ilikuwa imefungwa imara kwa ndani kwa kuwazuia Waisraeli wasiingie. Hakuna mutu aliyeweza kuingia wala kutoka katika muji huo. Yawe akamwambia Yoshua: “Mimi nitautia katika mikono yako muji wa Yeriko pamoja na mufalme wake na waaskari wake shujaa. Wewe na wale watu wenye silaha wote mutauzunguka ule muji mara moja kila siku kwa muda wa siku sita. Makuhani saba, kila mumoja akiwa anabeba baragumu yake ya pembe ya kondoo dume, watatangulia mbele ya Sanduku la Agano. Katika siku ya saba mutauzunguka muji ule mara saba, nao makuhani wakipiga mabaragumu. Watakapopiga hayo mabaragumu kwa mulio mukubwa na mara tu mutakaposikia huo mulio, watu wote watapiga kelele kubwa, nazo kuta za muji zitaanguka chini. Halafu watu wataushambulia muji kila mumoja kutoka pahali aliposimama.” Basi, Yoshua mwana wa Nuni, akawaita makuhani, akawaambia: “Mulibebe Sanduku la Agano na makuhani saba watwae mabaragumu saba ya kondoo dume, watangulie mbele ya Sanduku la Yawe.” Yoshua akawaambia watu: “Mupite mbele, muzunguke muji, nao watu wenye silaha waende mbele ya Sanduku la Agano la Yawe.” Kulingana na amri ya Yoshua, wale makuhani saba waliokuwa na mabaragumu saba ya kondoo dume wakaenda mbele ya Yawe, wakiwa wanapiga mabaragumu, nyuma yao wakifuatwa na lile Sanduku la Agano. Wale watu wenye silaha wakawatangulia wale makuhani ambao walikuwa wanapiga mabaragumu, na walinzi wengine wakifuata nyuma ya Sanduku hilo, nayo mabaragumu yakilia kwa mufululizo. Lakini Yoshua akawaamuru watu: “Musipige kelele au kutoa sauti, wala neno lolote lisitoke katika vinywa vyenu, mpaka siku ile ambapo nitawaambia mupige kelele; wakati ule ndipo mutakapopiga kelele.” Basi, Yoshua akawaamuru wale watu wauzunguke muji mara moja kila siku wakiwa wanabeba Sanduku la Agano la Yawe na kurudi katika kambi kulala usiku. Asubui yake Yoshua akaamuka mapema sana, na makuhani wakalibeba lile Sanduku la Agano la Yawe. Wale makuhani saba wenye mabaragumu saba ya kondoo dume walitembea mbele ya Sanduku la Yawe wakipiga mabaragumu kwa mufululizo. Watu wenye silaha walilitangulia Sanduku la Yawe na walinzi wengine nyuma yake. Mabaragumu yakaendelea kupigwa. Kwa siku ya pili, waliuzunguka ule muji mara moja; na kurudi tena katika kambi kwao. Wakafanya hivyo kwa muda wa siku sita. Siku ya saba, waliamuka asubui mapema, wakauzunguka muji ule mara saba. Ilikuwa ni siku hiyo tu ambayo waliuzunguka muji ule mara saba. Ilipofika mara ya saba, wakati makuhani walipokwisha kupiga mabaragumu, Yoshua akawaambia watu: “Mupige kelele, kwa kuwa Yawe amekwisha kuwapa huu muji! Muji ule utaangamizwa na kila kitu kinachokuwa mule maana umetolewa kwa Yawe. Rahabu, yule kahaba, ndiye atakayeachwa pamoja na wale ambao wako ndani ya nyumba yake kwa sababu aliwaficha wapelelezi wetu. Lakini musitwae kitu chochote ambacho kimetolewa kusudi kiangamizwe. Mukitwaa kitu chochote ambacho kimetolewa kusudi kiangamizwe, mutaifanya kambi ya Israeli kuwa kitu cha kuangamizwa, na hivyo kuiletea hasara. Lakini feza yote, zahabu, vyombo vya shaba na chuma ni vitakatifu kwa Yawe; hivyo vitawekwa katika hazina ya Yawe.” Basi, watu wakapiga kelele nayo mabaragumu yakiwa yanapigwa. Watu waliposikia sauti ya mabaragumu walipiga kelele kubwa, na kuta za muji zikaanguka chini kabisa. Mara tu watu wakaushambulia muji, kila mumoja kutoka pahali aliposimama, wakauteka. Kisha wakaangamiza kila kitu katika muji ule na kuwaua kwa upanga: wanaume na wanawake, vijana na wazee, ngombe, kondoo na punda. Yoshua akawaambia wale wapelelezi wawili walioipeleleza inchi hiyo: “Muende katika nyumba ya yule kahaba; mumulete yule mwanamuke na wale wote ambao ni wandugu zake kama mulivyomwapia.” Basi, wale vijana wapelelezi wakaenda; wakamuleta Rahabu, baba yake na mama yake, wandugu zake na watu wote wa jamaa yake, wakawaweka inje ya kambi ya Israeli. Kisha, wakauchoma kwa moto muji wa Yeriko na kila kitu kilichokuwa mule isipokuwa feza, zahabu, vyombo vya shaba na vya chuma; hivyo viliwekwa katika hazina ya nyumba ya Yawe. Lakini yule kahaba Rahabu pamoja na watu wote wa nyumba ya baba yake, Yoshua akayaokoa maisha yao. Rahabu akaishi kati ya Waisraeli mpaka leo, kwa sababu aliwaficha wajumbe ambao Yoshua aliwatuma kwenda kuupeleleza muji wa Yeriko. Wakati ule Yoshua akaapa mbele ya watu akisema: “Atakayeujenga tena muji wa Yeriko, alaaniwe na Mungu. Yeyote atakayeweka musingi wa muji huo, muzaliwa wake wa kwanza akufe. Yeyote atakayejenga mulango wa muji huo, mwana wake kitenda mimba akufe.” Basi, Yawe alikuwa pamoja na Yoshua na sifa zake zikaenea katika inchi yote. Lakini Waisraeli hawakukuwa waaminifu juu ya vile vitu vilivyotolewa viangamizwe maana Akana mwana wa Karmi, mujukuu wa Zabedi, wa ukoo wa Zera, wa kabila la Yuda, alitwaa vimoja kati ya vitu vilivyoamriwa viteketezwe. Kwa hiyo hasira ya Yawe ikawaka juu ya Waisraeli. Yoshua akawatuma watu kutoka Yeriko kwenda muji wa Ai, unaokuwa karibu ya Beti-Aweni, upande wa mashariki wa Beteli, akawaambia: “Mwende muipeleleze inchi.” Nao wakaenda na kuupeleleza muji wa Ai. Waliporudi, wakamwambia Yoshua: “Hakuna lazima ya kupeleka watu wote kuushambulia muji wa Ai, maana wakaaji wake ni wachache tu. Watu elfu mbili au tatu watatosha.” Basi, watu kama elfu tatu hivi wakaenda kuushambulia muji wa Ai, lakini wakakimbizwa na wakaaji wa muji huo. Watu wa Ai wakawaua Waisraeli makumi tatu na sita na kuwafukuza wengine kutoka mulango wa muji mpaka Sebarimu, wakawaua kwenye muteremuko. Waisraeli wakavunjika moyo na kuregea kama maji. Yoshua akapasua nguo yake, yeye pamoja na wazee wa Israeli. Wakajitupa chini ya Sanduku la Yawe mpaka magaribi; wakajitia mavumbi juu ya vichwa vyao. Yoshua akasema: “Ole wetu, ee Bwana wetu Yawe! Kwa nini umetuvukisha muto Yordani kwa kututia katika mikono ya Waamori kusudi watuangamize? Tungalifurahi kubaki ngambo ya muto Yordani! Ee Bwana, niseme nini wakati Waisraeli wamewakimbia waadui zao? Basi, Wakanana pamoja na wakaaji wote wa inchi hii watakapopata habari hiyo watatuzunguka na kutufuta kabisa katika dunia. Sasa utafanya nini kwa kuonyesha ukubwa wa jina lako?” Yawe akamwambia Yoshua: “Simama! Mbona umejitupa chini hivyo? Waisraeli wametenda zambi, maana wamelivunja agano langu nililowaamuru washike. Wametwaa vimoja kati ya vitu vilivyotolewa viangamizwe. Wameviiba na kudanganya, wakaviweka pamoja na vitu vyao. Kwa hiyo Waisraeli hawawezi kuwashinda waadui zao. Wanawakimbia waadui zao kwa sababu wamejifanya wenyewe kuwa kitu cha kuangamizwa! Sitakuwa pamoja nao tena musipoharibu vitu vinavyokuwa kati yenu vilivyotolewa viangamizwe. Basi, simama uwatakase watu, uwaambie wajitakase na kujitayarisha kwa siku ya kesho, maana mimi Yawe, Mungu wa Israeli, ninasema hivi: ‘Kati yenu kuna vitu vilivyotolewa viangamizwe. Hamuwezi kuwashinda waadui zenu mpaka vitu hivyo vimeondolewa kati yenu! Kwa hiyo kesho asubui wote mutakuja mbele yangu, kabila kwa kabila. Kabila nitakalolichagua litakwenda mbele, ukoo kwa ukoo. Ukoo nitakaouchagua utakwenda mbele, jamaa kwa jamaa. Na jamaa nitakayoichagua itakwenda mbele, mutu mumoja mumoja. Mutu yeyote atakayepatikana akiwa na vitu vilivyotolewa viangamizwe atateketezwa kwa moto, yeye pamoja na kila kitu chake maana ameliasi agano langu mimi Yawe, akatenda jambo la haya katika Israeli.’ ” Basi, Yoshua akaamuka asubui mapema, akawaleta Waisraeli wote karibu, kabila kwa kabila. Kabila la Yuda likachaguliwa. Akazileta karibu ukoo za Yuda, ukoo kwa ukoo; na ukoo wa Zera ukachaguliwa. Akazileta karibu jamaa za ukoo wa Zera, jamaa kwa jamaa; na jamaa ya Zabedi ikachaguliwa. Yoshua akaileta jamaa ya Zabedi karibu, nyumba kwa nyumba; na nyumba ya Akana mwana wa Karmi, mujukuu wa Zabedi mwana wa Zera, wa kabila la Yuda, ikachaguliwa. Yoshua akamwambia Akana: “Mwana wangu, umutukuze Yawe, Mungu wa Israeli, umusifu na kisha uniambie yale uliyotenda, wala usinifiche.” Akana akamujibu: “Ni kweli nimetenda zambi mbele ya Yawe, Mungu wa Israeli. Na hivi ndivyo nilivyofanya: Nilipoona vazi moja zuri kutoka Sinari kati ya vitu tulivyonyanganya, vikoroti mia mbili vya feza na furushi ya zahabu yenye uzito wa vikoroti makumi tano vya feza, nikavitamani na kuvitwaa; nikavificha katika udongo ndani ya hema langu; na feza iko chini ya vitu hivyo.” Basi, Yoshua akawatuma wajumbe, nao wakakimbia kwenye hema kwa Akana. Na kumbe, vitu vilikuwa vimefichwa katika hema na feza ikiwa chini yake. Wakavitwaa toka katika hema na kuvipeleka kwa Yoshua na watu wote wa Israeli; nao wakaviweka chini, mbele ya Yawe. Yoshua pamoja na Waisraeli wote, wakamukamata Akana mwana wa Zera, pamoja na feza, nguo, zahabu, watoto wake wa kiume na wabinti zake, ngombe, punda na kondoo wake, hema lake na kila kitu alichokuwa nacho na kuwapeleka kwenye bonde la Akori. Yoshua akamwuliza Akana: “Kwa nini umetuletea taabu? Yawe atakuletea taabu wewe mwenyewe leo.” Waisraeli wote wakamupiga Akana kwa mawe mpaka akakufa. Kisha wakawapiga jamaa yake yote kwa mawe mpaka wakakufa, wakawateketeza wote kwa moto. Halafu wakalundika mawe mengi juu yake, ambayo yako mpaka leo. Hapo hasira ya Yawe ikapoa; na pahali pale pakaitwa Bonde la Akori, ni kusema Bonde la Taabu, mpaka hivi leo. Yawe akamwambia Yoshua: “Usiogope, wala usikuwe na wasiwasi wowote; uwatwae waaskari wako wote uelekee muji wa Ai, maana nimetia mufalme wa Ai katika mikono yako, pamoja na watu wake, muji wake na inchi yake. Mutautendea muji wa Ai pamoja na mufalme wake kama vile mulivyoutendea muji wa Yeriko pamoja na mufalme wake. Mali zake pamoja na nyama wake mutakayoteka itakuwa ni mali yenu. Muende muushambulie muji kutoka upande wa nyuma.” Basi, Yoshua akaondoka, pamoja na waaskari wake wote kwenda Ai. Akawachagua watu hodari elfu makumi tatu na kuwaambia watangulie wakati wa usiku. Akawaamuru hivi: “Ninyi mutauvizia muji kutoka upande wa nyuma. Musiende mbali na muji, lakini mukuwe tayari wakati wote. Mimi, pamoja na watu wote wanaokuwa pamoja nami, tutaukaribia muji. Watakapotoka inje kuja kutushambulia kama pale mbele, sisi tutawakimbia. Nao wataendelea kutufuatilia mpaka wakuwe mbali na muji wao, maana watafikiri kwamba wanatukimbiza kama vile walivyofanya mbele. Sisi tutawaacha watufukuze. Hapo, ninyi mutatokea kutoka kule mulikokuwa munavizia na kuuteka muji, maana Yawe, Mungu wenu, atautia muji huo katika mikono yenu. Mukisha kuteka muji mutauteketeza kwa moto, kama vile Yawe alivyoamuru. Hayo ndiyo maagizo mutakayofuata.” Basi, Yoshua akawaambia waende pahali pao pa kuvizia; nao wakajiweka upande wa magaribi wa muji wa Ai, kati ya muji wa Ai na Beteli. Lakini Yoshua akalala usiku huo katika kambi ya Waisraeli. Yoshua akaamuka asubui mapema, akawakusanya Waisraeli na kuelekea katika muji wa Ai, akiwa pamoja na wazee. Waaskari wote waliofuatana naye walikaribia muji na kupiga kambi upande wake wa kaskazini, ngambo ya bonde kuelekeana na muji wa Ai. Halafu akatwaa watu wengine elfu tano na kuwaweka wavizie kati ya muji wa Beteli na Ai, upande wa magaribi wa muji wa Ai. Kundi kubwa liliwekwa upande wa kaskazini wa muji na wale waliobaki waliwekwa upande wa magaribi wa muji. Lakini usiku ule, Yoshua akalala katika bonde. Mufalme wa muji wa Ai alipoona hivyo, alifanya haraka na kwenda kwenye muteremuko wa kuelekea Araba kwa kushambulia Waisraeli katika vita. Lakini hakujua kwamba muji wake ulikuwa umeviziwa kutoka nyuma. Kisha Yoshua pamoja na watu wake wakajifanya sawa wenye kushindwa, wakaanza kukimbia kuelekea katika jangwa. Watu wote waliokuwa katika muji wakaitwa wawafuatilie Waisraeli; na walipokuwa wanamufuatilia Yoshua, walitoka na kwenda mbali na muji wao. Hakuna mutu yeyote aliyebaki katika muji wa Ai, waliuacha muji ule wazi wakaenda kuwafuatilia Waisraeli. Halafu Yawe akamwambia Yoshua: “Elekeza mukuki wako kule katika muji wa Ai maana nitautia muji ule katika mikono yako.” Yoshua akaelekeza mukuki wake kwenye muji wa Ai. Mara tu Yoshua alipouelekeza mukuki wake kule Ai, kundi lililokuwa likivizia upande mwingine likatoka na kuingia katika muji. Likauteka muji na kuuteketeza kwa moto. Watu wa Ai walipoangalia nyuma, wakaona moshi ukitoka katika muji ukipanda mpaka mbinguni. Nao hawakukuwa na uwezo wa kukimbia upande wowote, maana Waisraeli waliwageukia wale waliokuwa wanawafuatilia. Yoshua na Waisraeli wote walipoona kwamba kundi lililokuwa linavizia limeuteka muji, na kwamba moshi ulikuwa unapanda juu, waliwageukia na kuanza kuwaua. Watu waliobaki katika muji walitoka, lakini wote wakakuwa wamezungukwa na Waisraeli; nao wakauawa, wala hakukubaki hata mumoja wao. Lakini mufalme wa muji wa Ai walimuteka akiwa muzima na kumupeleka kwa Yoshua. Waisraeli walipomaliza kabisa kuwaua watu wote wa Ai kule katika jangwa ambako waliwafuatilia wakarudi katika muji wa Ai na kuwaua wote waliobaki mule. Jumla ya watu wa Ai waliouawa siku hiyo, wanaume na wanawake, walikuwa elfu kumi na mbili. Yoshua hakuushusha mukono wake aliokuwa akishikilia nao mukuki wake kuelekea Ai mpaka alipowaua wakaaji wote wa muji huo. Waisraeli waliteka tu nyama na mali kama vile Yawe alivyomwamuru Yoshua. Basi, Yoshua aliuteketeza muji wa Ai kwa moto na kuufanya mabomoko mpaka hivi leo. Kisha akamutundika mufalme wa Ai juu ya muti wa tini mpaka magaribi. Lakini jua lilipoanza kutua, Yoshua aliamuru maiti yake iondolewe juu ya muti na kutupwa kwenye mulango wa muji kisha walundike lundo kubwa la mawe juu ya maiti hiyo. Lundo hilo liko kule mpaka leo. Kisha, Yoshua akamujengea Yawe, Mungu wa Israeli, mazabahu juu ya mulima Ebali, kama vile Musa mutumishi wa Yawe alivyowaagiza Waisraeli, kadiri ilivyoandikwa katika kitabu cha Sheria ya Musa kwamba itakuwa mazabahu iliyojengwa kwa mawe ambayo hayakuchongwa, wala kuguswa na chombo chochote cha chuma. Juu ya mazabahu hiyo wakamutolea Yawe sadaka za kuteketezwa kwa moto na sadaka za amani. Na kule, mbele ya Waisraeli wote, Yoshua aliandika mufano wa sheria ya Musa juu ya mawe. Waisraeli wote pamoja na viongozi wao, wazee na waamuzi na wageni wote waliokuwa kati yao, wakasimama kila upande kuelekeana na Sanduku la Agano mbele ya makuhani Walawi waliokuwa wamelibeba Sanduku la Agano la Yawe. Nusu yao wakasimama mbele ya mulima Gerizimu na nusu nyingine wakasimama mbele ya mulima Ebali, kama vile Musa, mutumishi wa Yawe alivyoagiza pale mbele juu ya kubarikiwa kwa Waisraeli. Kisha, Yoshua akawasomea sheria zote, pamoja na baraka na laana kama ilivyoandikwa katika kitabu cha sheria. Hakuna neno lililoamriwa na Musa ambalo Yoshua hakulisoma mbele ya Waisraeli, kati yao kukiwa wanawake, watoto na wageni. Wafalme wote waliokuwa ngambo ya muto Yordani katika inchi ya milima na kwenye mabonde na eneo lote la pembeni ya bahari ya Mediteranea kuelekea Lebanoni, Wahiti, Waamori, Wakanana, Waperizi, Wahivi na Wayebusi waliposikia habari za Waisraeli, wakakusanyika pamoja kwa nia moja kwa kupigana vita na Yoshua na Waisraeli. Lakini wakaaji wa Gibeoni walipopata habari juu ya jinsi Yoshua alivyoitendea miji ya Yeriko na Ai, waliamua kutumia werevu. Wakatayarisha vyakula, wakapakiza magunia yaliyochakaa juu ya punda wao, vibuyu vilivyochakaa na kushonwa. Wakavaa viatu, nguo zilizochakaa na vyakula vyao vyote vilikuwa vimekauka na kuota manyoya. Basi, wakamwendea Yoshua katika kambi kule Gilgali, wakamwambia yeye na Waisraeli: “Sisi tumetoka katika inchi ya mbali. Tafazali tunaomba mufanye agano nasi.” Lakini Waisraeli wakawajibu hao Wahivi: “Tunaweza namna gani kufanya agano nanyi? Labda ninyi munaishi karibu nasi.” Nao wakamwambia Yoshua: “Sisi tuko watumishi wako.” Naye Yoshua akawauliza: “Ninyi ni nani, na munatoka wapi?” Wakamujibu: “Sisi, watumishi wako, tumetoka inchi ya mbali na tumekuja kwa maana tumesikia sifa za jina la Yawe, Mungu wenu. Tulipata habari za utukufu wake na yote aliyoyafanya katika inchi ya Misri. Tumesikia yote aliyowatendea wafalme wawili wa Waamori waliokuwa ngambo ya muto Yordani, mufalme Sihoni wa Hesiboni na mufalme Ogi wa Basani aliyekaa kule Astaroti. Halafu wazee wetu na wanainchi wote wa inchi yetu, wakatuambia, tutayarishe posho ya safari, tukuje kukutana nanyi na kuwaambia kwamba sisi ni watumishi wenu. Tafazali mufanye agano nasi. Angalia mikate yetu ambayo ilikuwa bado moto tulipoibeba wakati tulipoondoka kwetu, lakini sasa imekauka na kuota manyoya. Vibuyu hivi tulivijaza maji vikiwa vipya, lakini sasa vimepasukapasuka. Hata nguo na viatu vyetu vimechakaa, maana safari ilikuwa ndefu sana.” Hivyo, Waisraeli wakatwaa vyakula vyao, bila kumwuliza Yawe shauri. Yoshua akafanya nao mapatano ya amani; akafanya agano kwamba atawaruhusu kuishi. Viongozi wa Waisraeli wakawaapia kutimiza mapatano hayo. Siku tatu nyuma ya kufanya agano nao, Waisraeli wakagundua kwamba watu hao walikuwa jirani zao na waliishi kati yao. Basi, Waisraeli wakafunga safari, nyuma ya siku ya tatu wakafika katika miji yao. Miji hiyo ilikuwa Gibeoni, Kefira, Beroti na Kiriati-Yearimu. Lakini Waisraeli hawakuwaua, maana viongozi wa Waisraeli walikuwa wamewaapia kwa jina la Yawe, Mungu wa Israeli. Hivyo basi, Waisraeli wote wakawanungunikia viongozi wao. Lakini viongozi wa Waisraeli wakawaambia watu wao: “Kwa vile tumewaapia kwa jina la Yawe, Mungu wa Israeli, sasa hatuwezi kuwazuru. Tutawaacha waishi, kusudi tusipate kuazibiwa kwa sababu ya kiapo tulichofanya. Muwaache waishi.” Hivyo Wagibeoni wakakuwa wanatumikia Waisraeli wakiwakatia kuni na kuwachotea maji, kama viongozi wa Waisraeli walivyosema. Yoshua akawaita Wagibeoni na kuwauliza: “Kwa nini mulitudanganya kwamba mulitoka inchi ya mbali na wakati ninyi munaishi kati yetu? Sasa, ninyi mumelaaniwa nanyi siku zote mutakuwa watumwa wa kukata kuni na kuchota maji kwa ajili ya nyumba ya Mungu wangu.” Wakamujibu Yoshua: “Tuliambiwa kwamba kwa hakika Yawe, Mungu wenu, alimwamuru mutumishi wake Musa awaangamize wakaaji wote wa inchi hii na kuwapa ninyi inchi hii ikuwe mali yenu. Kwa hivyo, tuliogopea maisha yetu na ndipo tukafanya jambo hili. Sasa sisi tuko katika mikono yako, ututendee kama unavyoona vema na haki.” Basi, jambo Yoshua alilowatendea ni kuwaokoa toka katika mikono ya Waisraeli kusudi wasiwaue. Lakini kutokea siku hiyo, Yoshua akawafanya hao kuwa wakata - kuni na wachota - maji kwa ajili ya Waisraeli wote na kwa ajili ya mazabahu ya Yawe, popote pale Yawe alipochagua mpaka hivi leo. Mufalme Adoni-Zedeki wa Yerusalema akapata habari juu ya jinsi Yoshua alivyouteka muji wa Ai na kuuharibu kabisa akiutendea muji huo na mufalme wake kama alivyoutendea Yeriko na mufalme wake. Vilevile akapata habari kwamba wakaaji wa Gibeoni walikuwa wamefanya mapatano ya amani na Waisraeli na kwamba sasa wanaishi kati yao. Habari hizo zilisababisha hofu kubwa kule Yerusalema kwa sababu muji wa Gibeoni ulikuwa mukubwa sana kati ya miji ya kifalme. Muji huu ulikuwa vilevile mukubwa kuliko Ai na wanaume wake wote walikuwa waaskari hodari sana. Basi, Mufalme Adoni-Zedeki akapeleka ujumbe kwa mufalme Hohamu wa Hebroni, mufalme Piramu wa Yarmuti, mufalme Yafia wa Lakisi na mufalme Debiri wa Eguloni, akawaambia: “Mukuje munisaidie tuwaangamize Wagibeoni, maana wamefanya mapatano ya amani na Yoshua pamoja na Waisraeli.” Kisha wafalme hao watano wa Waamori: mufalme wa Yerusalema, mufalme wa Hebroni, mufalme wa Yarmuti, mufalme wa Lakisi na mufalme wa Eguloni, wakaunganisha waaskari wao, wakaenda nao mpaka Gibeoni. Wakapiga kambi kuuzunguka muji huo, wakaushambulia. Wagibeoni wakapeleka ujumbe kwa Yoshua kule katika kambi Gilgali, wakamwambia: “Tafazali, usitutupilie sisi watumishi wako. Ukuje mbio utusaidie na kutuokoa kwa maana wafalme wote wa Waamori kutoka inchi ya milima wamekuja kutushambulia.” Basi, Yoshua pamoja na jeshi lake lote na mashujaa wakaondoka Gilgali. Yawe akamwambia Yoshua: “Usiwaogope hata kidogo maana nimewatia katika mikono yako, wala hakuna hata mumoja atakayeweza kukushinda.” Nyuma ya kutembea kutoka Gilgali usiku kucha, Yoshua akawatokea kwa rafla. Naye Yawe akawatia hofu kubwa mbele ya Waisraeli ambao waliwaua watu wengi kule Gibeoni wakiwakimbia kwenye njia ya muteremuko wa Beti-Horoni mpaka Azeka na Makeda ambako vilevile waliwaua watu wengi sana. Walipokuwa wakiwakimbia Waisraeli kwenye muteremuko wa Beti-Horoni, Yawe akawanyeshea mvua ya mawe makubwa kutoka mbinguni wakiwa katika njia mpaka Azeka hata waliouawa kwa mawe hayo wakakuwa wengi kuliko waliouawa kwa silaha za Waisraeli. Wakati Yawe alipowatia Waamori katika mikono ya Waisraeli, Yoshua alimwomba Yawe mbele ya Waisraeli wote, akasema: “Wewe jua, simama kimya juu ya Gibeoni, wewe mwezi, katika bonde la Ayaloni.” Jua likasimama kimya na mwezi ukasimama mpaka taifa la Israeli lilipolipiza kisasi waadui zake. Kama vile ilivyoandikwa katika kitabu cha Yaseri, jua lilisimama kimya katikati ya mbingu, likakatiza safari yake ya kwenda kutua kwa siku nzima. Hakujakuwa siku kama hiyo hata kidogo wala haijapata kuonekana tena, siku ambayo Yawe amemwitikia mwanadamu kwa namna hiyo; maana Yawe mwenyewe aliwapigania Waisraeli. Kisha Yoshua akarudi katika kambi kule Gilgali pamoja na Waisraeli wote. Wale wafalme watano wakakimbia na kujificha katika pango la Makeda. Yoshua akapata habari kwamba wafalme hao wamegunduliwa walikojificha katika pango la Makeda. Yoshua akasema: “Muviringishe mawe makubwa kwenye mulango wa pango na kuweka walinzi pale. Lakini ninyi musikae kule, muwafuatilie waadui zenu. Muwapige kutoka upande wa nyuma, wala musiwaache waingie katika miji yao, maana Yawe, Mungu wenu, amewatia katika mikono yenu.” Yoshua pamoja na Waisraeli wakawapiga na kuwaangamiza wote, na wachache wao walioponyoka wakakimbilia kwenye miji yao yenye kuta. Nyuma ya hayo Waisraeli wote wakarudi salama kwa Yoshua kule katika kambi Makeda; na hakuna tena mutu aliyesubutu kusema neno lolote juu ya Waisraeli. Kisha Yoshua akasema: “Mufungue mulango wa pango muniletee kutoka mule wale wafalme watano.” Wakafanya hivyo, wakamuletea Yoshua wale wafalme watano: mufalme wa Yerusalema, mufalme wa Hebroni, mufalme wa Yarmuti, mufalme wa Lakisi na mufalme wa Eguloni. Wafalme hao walipoletwa, Yoshua akawaita Waisraeli wote na wakubwa wa waaskari waliokwenda naye kwa vita, akawaambia: “Mukuje karibu muwakanyage wafalme hawa kwenye shingo yao.” Nao wakasogea na kuwakanyaga kwenye shingo. Yoshua akawaambia: “Musiogope, wala musikuwe na wasiwasi, mukuwe imara na hodari, maana hivi ndivyo Yawe atakavyowatendea waadui zenu ambao mutapigana nao. Kwa hiyo, mukuwe imara na hodari.” Kisha, Yoshua aliwanyonga kwa kuwatundika kwenye miti mitano ambako walitundikwa mpaka magaribi. Wakati jua lilipokuwa karibu kutua, Yoshua aliamuru waondolewe juu ya miti walipokuwa wametundikwa na kutupwa katika pango walimokuwa wamejificha. Kisha wakaweka mawe makubwa kwenye mulango wa pango, nayo mawe hayo yako kule mpaka leo. Siku hiyo Yoshua alipouteka muji wa Makeda, alimuua mufalme wake na wakaaji wake wote bila kuacha hata mutu mumoja. Alimutendea mufalme wa Makeda kama vile alivyomutendea mufalme wa Yeriko. Kutoka Makeda, Yoshua pamoja na Waisraeli wote walikwenda Libuna wakaushambulia. Yawe akautia muji huo pamoja na mufalme wao katika mikono ya Waisraeli, wakawaua wakaaji wake bila kuacha hata mutu mumoja. Walimutendea mufalme wa Libuna kama vile walivyomutendea mufalme wa Yeriko. Kisha kutoka Libuna Yoshua na Waisraeli wote walikwenda Lakisi, wakauzunguka muji ule na kuushambulia. Naye Yawe akautia muji huo katika mikono ya Waisraeli, wakauteka kisha siku mbili. Waliwaua wakaaji wote wa muji huo kama walivyofanya kule Libuna. Hapo, mufalme Horamu wa Gerezi akaamua kuja kuwasaidia watu wa Lakisi. Lakini Yoshua akamwua pamoja na watu wake wote, hakuacha hata mutu mumoja. Kisha kutoka Lakisi, Yoshua na Waisraeli wote walikwenda mpaka Eguloni, wakauzunguka muji ule na kuushambulia. Wakauteka siku hiyohiyo na kuwaua wakaaji wake wote kama walivyofanya kule Lakisi. Halafu kutoka Eguloni Yoshua na Waisraeli wote wakaenda mpaka Hebroni, wakaushambulia na kuuteka. Wakawaua wakaaji wake wote pamoja na mufalme wao; waliiharibu kabisa miji mingine iliyouzunguka, wakawaua wakaaji wake wote kama walivyofanya kule Eguloni. Kisha, Yoshua na Waisraeli wote wakarudi Debiri, wakaushambulia muji ule. Waliuteka muji huo na mufalme wake pamoja na miji mingine yote iliyouzunguka na kuwaangamiza wote waliokuwa ndani yao bila kuacha hata mutu mumoja. Waliutendea muji huo kama walivyoutendea muji wa Hebroni na muji wa Libuna na wafalme wao. Basi, Yoshua aliiteka inchi yote; akawashinda wafalme wa sehemu za milima, eneo la Negebu, na sehemu za inchi ya bonde na miteremuko. Hakuacha kitu chochote chenye uzima lakini aliangamiza kila kitu kama vile Yawe, Mungu wa Israeli, alivyoamuru. Yoshua akawashinda watu wote kutokea Kadesi-Barnea mpaka Gaza, na kutokea Goseni mpaka Gibeoni. Aliweza kuitwaa inchi hii yote kwa sababu Yawe, Mungu wa Israeli, aliwapigania Waisraeli. Basi, Yoshua akarudi mpaka katika kambi kule Gilgali pamoja na Waisraeli wote. Mufalme Yabini wa muji wa Hazori alipopata habari hizo, alipeleka ujumbe kwa mufalme Yobabu wa Madoni, kwa mufalme wa Simuroni na mufalme wa Akisafu, na kwa wafalme waliokuwa katika milima ya upande wa kaskazini, waliokuwa Araba ambayo ilikuwa upande wa kusini wa Kineroti, kwenye mabonde na waliokuwa Nafoti-Dori katika upande wa magaribi. Vilevile, akapeleka ujumbe kwa Wakanana waliokuwa pande za mashariki na magaribi, kwa Waamori, Wahiti, Waperizi, Wayebusi ambao walikaa katika milima na kwa Wahivi ambao walikaa chini ya mulima Hermoni katika inchi ya Misipa. Basi, wakatoka wote na makundi yao makubwa ya waaskari. Nao walikuwa wengi kama muchanga wa bahari pamoja na magari mengi na farasi wengi sana. Wafalme hawa wote wakaungana na kupiga kambi yao katika chemichemi ya Meromu kusudi wapigane na Waisraeli. Yawe akamwambia Yoshua: “Usiwaogope hao, maana kesho, wakati kama huu, nitawaangamiza wote kwa kuwatia katika mikono ya Waisraeli; nanyi mutakata mishipa ya miguu ya farasi wao na kuteketeza magari yao kwa moto.” Basi, kwa rafla kwenye chemichemi ya Meromu, Yoshua pamoja na waaskari wake wote akawatokea na kuwashambulia. Yawe akawatia katika mikono ya Waisraeli, nao wakawashinda na kuwafukuza mpaka Sidona muji mukubwa na Misirepotaimu, mpaka upande wa mashariki katika bonde la Misipa. Waisraeli wakawapiga na kuwaua wote. Yoshua akakatakata mishipa ya miguu ya farasi wao wote na kuyateketeza magari yao kwa moto, kama Yawe alivyomwagiza. Yoshua alipokuwa anarudi, akauteka muji wa Hazori. Akamwua mufalme wake maana ndiye aliyekuwa kiongozi wa falme hizo zote. Kisha akauteketeza muji wa Hazori kwa moto na kuwaua wakaaji wake wote, hakumwacha hata mutu mumoja. Vilevile aliiteketeza miji ile mingine yote kwa moto na kuwaua wafalme wao wote kama vile Musa, mutumishi wa Yawe, alivyomwamuru. Lakini Waisraeli hawakuiteketeza miji iliyokuwa kwenye vilima, isipokuwa tu muji wa Hazori ambao Yoshua aliuteketeza. Waisraeli wakatwaa vitu vyote walivyonyanganya na nyama wa miji hiyo; lakini waliwaua wakaaji wake wote, wala hawakumwacha hata mutu mumoja. Musa mutumishi wa Yawe aliipewa amri hii, naye Musa akamwamuru Yoshua ambaye aliitimiza. Yoshua alitimiza kila jambo Yawe alilomwamuru Musa. Yoshua aliiteka inchi nzima: sehemu za milima na sehemu zote za kusini, eneo lote la Goseni, inchi ya mabonde, inchi ya Araba, milima ya Israeli na sehemu zake za mabonde; aliwateka na kuwaua wafalme wote wa inchi hizo kuanzia kwenye mulima uliokuwa mutupu wa Halaki karibu na Seiri mpaka Bali-Gadi katika bonde la Lebanoni, upande wa kusini wa mulima Hermoni. Vita Yoshua aliyopigana na wafalme hawa wote ilikamata muda murefu. Hakuna muji ambao ulifanya mapatano ya amani na Waisraeli, isipokuwa Gibeoni tu, ambamo Wahivi waliishi. Waisraeli waliiteka miji mingine yote kwa kupigana vita. Ilikuwa ni mapenzi ya Yawe mwenyewe kuifanya mioyo ya watu wa mataifa hayo kuwa migumu kusudi wapigane. Alikusudia wasihurumiwe lakini wateketezwe. Ndivyo Yawe alivyomwamuru Musa. Wakati ule, Yoshua akakwenda, akawaangamiza Waanaki waliokuwa wanaishi katika milima kule Hebroni, Debiri, Anabu, inchi yote ya milima ya Yuda na Israeli. Yoshua akawaangamiza watu hao pamoja na miji yao. Hakuna mutu wa kabila la Anaki ambaye alibakia katika inchi ya Israeli; walibaki wachache tu katika miji ya Gaza, Gati na Asidodi. Basi, Yoshua akaitwaa inchi yote kulingana na yote yale Yawe aliyomwambia Musa. Yoshua akaipatia Waisraeli ikuwe mali yao, wagawanyane kulingana na makabila yao. Kisha inchi nzima ikatulia, ikakuwa haina vita tena. Hawa ndio wafalme ambao Waisraeli waliwashinda na kunyanganya inchi yao yote iliyokuwa upande wa mashariki wa muto Yordani kutokea bonde la muto Arnoni mpaka kwenye mulima Hermoni na inchi yote ya Araba upande wa mashariki: Mufalme Sihoni wa Waamori aliyeishi kule Hesiboni na kutawala kutokea kwenye makao yake makubwa kule Aroeri, muji uliokuwa kandokando ya bonde la Arnoni. Alitawala vilevile kuanzia katikati ya bonde mpaka kwenye muto Yaboki ambao ulikuwa mupaka wa inchi ya Waamoni, ni kusema nusu ya inchi ya Gileadi. Vilevile, alitawala inchi yote ya Araba, kutokea bahari ya Kineroti, upande wa mashariki, mpaka Beti-Yesimoti kwenye bahari ya Chumvi na kuendelea mpaka chini ya mulima Pisiga. Mwingine ni mufalme Ogi mumoja wa Warefaimu waliobaki, ambaye alitawala Basani na alikaa Asitaroti au Edirei. Utawala wake ulienea mpaka kule kwenye mulima Hermoni, kule Saleka, Basani yote mpaka kwa mipaka ya Wagesuri na Wamakati, nusu ya Gileadi hata kwa mupaka wa inchi ya mufalme Sihoni wa Hesiboni. Musa mutumishi wa Yawe pamoja na Waisraeli aliwashinda wafalme hao, akawapatia inchi hizo makabila ya Rubeni, Gadi na nusu ya kabila la Manase zikuwe mali yao kabisa. Kisha Yoshua pamoja na Waisraeli waliwashinda wafalme wote wa eneo lote linalokuwa upande wa magaribi wa muto Yordani, kuanzia Bali-Gadi katika bonde la Lebanoni mpaka kwenye mulima uliokuwa mutupu wa Halaki upande wa kusini karibu na Seiri. Yoshua akayagawanyia makabila ya Israeli inchi hizo zikuwe mali yao kabisa. Inchi hizo zilikuwa pamoja na maeneo ya milima, inchi ya bonde, eneo la Araba, miteremuko ya milima, maeneo ya jangwa, na eneo la Negebu; inchi zilizokuwa za Wahiti, Waamori, Wakanana, Waperizi, Wahivi na Wayebusi. Wafalme walioshindwa walikuwa, mumoja kwa mwengine: mufalme wa Yeriko, mufalme wa Ai muji unaokuwa karibu na Beteli, mufalme wa Yerusalema, mufalme wa Hebroni, mufalme wa Yarmuti, mufalme wa Lakisi, mufalme wa Eguloni, mufalme wa Gezeri, mufalme wa Debiri, mufalme wa Gederi, mufalme wa Horma, mufalme wa Aradi, mufalme wa Libuna, mufalme wa Adulamu, mufalme wa Makeda, mufalme wa Beteli, mufalme wa Tapua, mufalme wa Heferi, mufalme wa Afeki, mufalme wa Lasaroni, mufalme wa Madoni, mufalme wa Hazori, mufalme wa Simuroni-Meroni, mufalme wa Akisafu, mufalme wa Tanaki, mufalme wa Megido, mufalme wa Kedesi, mufalme wa Yokinamu muji unaokuwa kwenye mulima Karmeli, mufalme wa Dori katika sehemu ya Nafoti-Dori, mufalme wa Goyimu kule Gilgali na mufalme wa Tirza. Jumla ya wafalme hao ni makumi tatu na mumoja. Wakati huu, Yoshua alikuwa muzee wa miaka mingi. Basi, Yawe akamwambia: “Wewe sasa umekuwa muzee wa miaka mingi, na kumebaki bado sehemu kubwa za inchi ambazo hazijatwaliwa. Sehemu hizo ni: inchi yote ya Wafilistini na inchi yote ya Wagesuri, ni kusema eneo linalojulikana kama la Wakanana, kuanzia kwenye kijito cha Sihori kwa mupaka wa Misri mpaka kwenye eneo la Ekuroni kule kaskazini. Maeneo yote ya watawala watano wa Wafilistini: Gaza, Asidodi, Asikeloni, Gati na Ekuroni pamoja na eneo la Awini, upande wa kusini. Vilevile inchi za Wakanana kuanzia Ara ya Wasidoni mpaka Afeki kwa mupaka wa Waamori; vilevile eneo la Gebali na Lebanoni upande wa mashariki ya Bali-Gadi chini ya mulima Hermoni mpaka Lebo-Hamati; vilevile eneo la milima inayokuwa kati ya Lebanoni na Misirepoti-Maimu ambayo wakaaji wake ni Wasidoni. Kadiri na jinsi Waisraeli watakavyoendelea mbele, mimi mwenyewe nitayafukuza mataifa hayo katika inchi hizo mbele yao. Nawe utawagawanyia Waisraeli sehemu mbalimbali za inchi hizo kwa kura kama nilivyokuamuru. Utayagawanyia inchi hizo makabila kenda na nusu ya kabila la Manase ambao bado hawajapata kitu.” Makabila ya Rubeni, Gadi na nusu nyingine ya kabila la Manase yalikuwa yamepewa inchi inayokuwa upande wa mashariki wa muto Yordani, kama vile Yawe alivyomwamuru Musa, mutumishi wake. Eneo lao lilikuwa kuanzia Aroeri kandokando ya bonde la Arnoni na muji ule unaokuwa katikati ya bonde, na inchi ile yote ya bonde tangu Medeba mpaka Diboni, pamoja na miji ya mufalme Sihoni wa Waamori, aliyetawala kule Hesiboni hata kwa mupaka wa Waamoni, pamoja na inchi za Gileadi, eneo la Wagesuri na Wamakati mulima wa Hermoni na inchi yote ya Basani mpaka Saleka; na ufalme wote wa Ogi mumoja wa Warefaimu waliobaki, ambaye alitawala kule Asitaroti na Edirei katika Basani. Musa alikuwa amewashinda hao wote na kuwafukuzia mbali. Hata hivyo, Wagesuri na Wamakati hawakufukuzwa lakini wanaishi kati ya Waisraeli mpaka leo. Musa hakuwapa watu wa kabila la Lawi inchi yoyote. Lakini sadaka za kuteketezwa kwa moto walizomutolea Yawe, Mungu wa Israeli, hizo ndizo zilizokuwa fungu lao, kama vile Yawe alivyomwambia Musa. Sehemu ya inchi ambayo Musa aliwapa watu wa kabila la Rubeni kulingana na jamaa zao, ilikuwa kuanzia Aroeri pembeni ya bonde la Arnoni na muji uliokuwa katika bonde hilo pamoja na inchi yote ya bonde ya Medeba. Ilikuwa vilevile pamoja na Hesiboni na miji yake yote inayokuwa katika sehemu ya bonde: ni kusema Diboni, Bamoti-Bali, Beti-Bali-Meoni, Yasa, Kedemoti, Mefati, Kiriataimu, Sibuma, Zereti-Sahari, kule kwa kilima katika bonde, Beti-Peori, miteremuko ya mulima Pisiga, Beti-Yesimoti na miji yote ya mabonde, inchi yote ya mufalme Sihoni wa Waamori ambaye alitawala kule Hesiboni; Musa alikuwa amemushinda huyu Sihoni pamoja na viongozi wa Midiani, Evi, Rekemu, Suri, Huri na Reba, ambao walitawala inchi kwa jina la mufalme Sihoni. Balamu mwaguzi mwana wa Beori ambaye Waisraeli walimwua alikuwa mumoja wao. Mupaka wa inchi ya kabila la Rubeni upande wa magaribi ulikuwa muto Yordani. Miji na maeneo yaliyotajwa hapa ndiyo sehemu waliyopewa watu wa ukoo za kabila la Rubeni. Sehemu ya inchi ambayo Musa aliwapa watu wa kabila la Gadi kulingana na ukoo zao ilikuwa Yazeri, miji yote ya Gileadi na nusu ya inchi ya Waamoni mpaka Aroeri kwa upande wa mashariki wa Raba. Vilevile kuanzia Hesiboni mpaka Ramati-Misipe, Betonimu, na kutokea Mahanaimu hata kwa mupaka wa Debiri. Vilevile miji iliyokuwa katika bonde la Beti-Haramu, Beti-Nimura, Sukoti na Zafoni na inchi yote iliyokuwa ya mufalme Sihoni wa Hesiboni; eneo hilo lilikuwa upande wa mashariki wa Yordani na kupakana na upande wa kusini wa bahari ya Kineroti. Miji na vijiji hivi ndivyo watu wa kabila la Gadi walivyopewa kulingana na ukoo zao. Tena, Musa alikuwa ameipatia nusu ya kabila la Manase kulingana na ukoo zake, eneo la inchi kuanzia Mahanaimu mpaka kuingia katika inchi yote iliyokuwa ya mufalme Ogi katika Basani, pamoja na miji makumi sita ya Yairi, nusu ya Gileadi, Astaroti, Edirei, ambayo ilikuwa ya mufalme Ogi wa Basani. Nusu ya wazao wa Makiri mwana wa Manase, eneo hili walipewa kulingana na ukoo zao. Musa alikuwa amewagawanyia sehemu hizo mbalimbali za inchi iliyokuwa upande wa mashariki wa Yeriko na Yordani, wakati alipokuwa kwenye mabonde ya Moabu. Lakini kabila la Lawi, Musa hakulipa sehemu yao ya inchi, maana aliwaambia kwamba sehemu yao itakuwa kumutumikia Yawe, Mungu wa Israeli. Haya ndiyo maeneo ya inchi ambayo Waisraeli walipewa katika inchi ya Kanana. Kuhani Eleazari na Yoshua mwana wa Nuni, pamoja na wakubwa wa ukoo za makabila ya Waisraeli waliyowagawanyia Waisraeli. Sehemu hiyo yao waligawanyiwa kwa kura kama vile Yawe alivyomwamuru Musa awape yale makabila tisa na nusu. Musa alikuwa ameyapa yale makabila mawili na nusu sehemu yao upande wa mashariki wa Yordani, lakini Walawi hawakukuwa wamepewa sehemu yao pamoja nao. Wazao wa Yosefu walikuwa makabila mawili: Manase na Efuraimu. Kabila la Lawi halikupewa sehemu yoyote ya inchi, lakini miji tu ya kuishi na mashamba ya malisho kwa ajili ya nyama wao na riziki zao. Basi, Waisraeli wakaigawanya inchi kama vile Yawe alivyomwamuru Musa. Siku moja watu wa kabila la Yuda wakamwendea Yoshua kule Gilgali. Kalebu mwana wa Yefune, ambaye alikuwa Mukenizi, akamwambia Yoshua: “Bila shaka unakumbuka jinsi Yawe alivyomwambia Musa, mutu wa Mungu, juu yangu na wewe tulipokuwa Kadesi-Barnea. Nilipokuwa na umri wa miaka makumi ine, Musa mutumishi wa Mungu, akanituma kutoka Kadesi-Barnea, kwenda kuipeleleza inchi. Niliporudi nikamuletea habari za mambo ya kule kadiri nilivyoamini katika moyo wangu. Wakati wale wenzangu waliokwenda pamoja nami waliwavunja watu moyo, lakini mimi nilimufuata Yawe, Mungu wangu, kwa uaminifu. Siku hiyo Musa akaniapia: ‘Hakika sehemu ya inchi ile ambayo ulipita ndani yake itakuwa yako wewe na wazao wako milele. Kwa sababu ya uaminifu wako kwa Yawe, Mungu wako’. Lakini sasa ni muda wa miaka makumi ine na mitano tangu Yawe aliposema na Musa, wakati Waisraeli walipokuwa wanapita katika jangwa. Tangu wakati ule Yawe, kama vile alivyoahidi, amenilinda muzima mpaka leo, na sasa mimi nina umri wa miaka makumi nane na mitano. Lakini bado nina nguvu kama nilivyokuwa wakati ule Musa aliponituma. Hata sasa nina nguvu za kuweza kupigana vita au kufanya kazi nyingine yoyote. Sasa ninaomba unipe inchi hii ya milima ambayo Yawe aliniahidi siku ile. Wewe ulisikia siku ile kwamba Waanaki waliishi humo katika miji yenye kuta; labda Yawe atakuwa pamoja nami, nami nitawafukuza kama vile Yawe alivyosema.” Halafu Yoshua akamubariki Kalebu mwana wa Yefune na kumupa muji wa Hebroni kuwa sehemu yake. Kwa hiyo, muji wa Hebroni ni sehemu yao wazao wa Kalebu mwana wa Yefune Mukenizi mpaka hivi leo, kwa sababu Kalebu alikuwa mwaminifu kwa Yawe, Mungu wa Israeli. Muji wa Hebroni zamani uliitwa Kiriati-Arba. Arba alikuwa mutu mukubwa kuliko wote kati ya Waanaki. Inchi nzima ikakuwa tulivu bila vita. Eneo la inchi watu wa kabila la Yuda walilopewa kwa kura kulingana na jamaa zake lilienea tangu kusini mashariki mpaka kwa mupaka wa Edomu. Sehemu ya kusini kabisa ilikuwa jangwa la Sini. Mupaka wao upande wa kusini ulianzia kwenye pembe ya kusini ya bahari ya Chumvi, ukaendelea kwa kusini mpaka kwenye mwinuko wa Akarabimu, ukapitia pembeni ya Sini, na kusini ya Kadesi-Barnea, ukipitia Hesironi hata Adari na kisha ukageuka kuelekea Karaka. Kutoka hapo ulipita karibu na Asimoni na kufuata kijito cha Misri mpaka kufikia kwenye bahari ya Mediteranea. Hapo ndipo mupaka wa kusini wa Yuda ulipopita. Mupaka wao wa upande wa mashariki ni bahari ya Chumvi mpaka pale muto Yordani unapoingilia katika bahari. Na mupaka wao upande wa kaskazini ulipita kutokea pembe ya bahari ya Chumvi pahali ambapo muto Yordani unaingilia katika bahari. Mupaka huo ukapita Beti-Hogla na kaskazini ya Beti-Araba mpaka kwenye jiwe la Bohani mwana wa Rubeni. Kutoka hapo, uliendelea mpaka Debiri kwenye bonde la Akori na kaskazini kuelekea Gilgali, karibu na mwinuko wa Adumimu ambao uko upande wa kusini wa kijito, kisha ukaelekea kwenye chemichemi za Eni-Semesi na kuishia Eni-Rogeli. Kisha, mupaka huo ulipitia kwenye Bonde la Hinomu, upande wa kusini wa kilima cha Wayebusi, ni kusema Yerusalema, kuelekea kilele cha mulima unaokuwa upande wa magaribi wa bonde la Hinomu na kufika mwisho wa bonde la Refaimu. Kutoka hapo, ulielekea kwenye mulima mpaka chemichemi za Nefutoa, mpaka kwenye miji ya mulima wa Efuroni. Hapo mupaka uligeuka na kuelekea Bala, ni kusema Kiriati-Yearimu, ambako ulipinda upande wa magaribi kuelekea Seiri; ukapita kaskazini ya mulima wa Yerimu, ni kusema Kesaloni, na kuteremuka mpaka Beti-Semesi ambapo ulipita karibu na Timuna. Kisha ukaendelea upande wa kaskazini wa Ekuroni, ukazunguka kuelekea Sikeroni ambapo ulipita karibu na mulima Bala mpaka Yabuneli ukaishia katika bahari ya Mediteranea. Mupaka wa upande wa magaribi ulikuwa bahari ya Mediteranea. Ndivyo ilivyokuwa mipaka ya eneo walilopewa watu wa kabila la Yuda kulingana na ukoo zao. Kalebu mwana wa Yefune, alipewa sehemu ya inchi ya Yuda kama vile Yawe alivyomwamuru Yoshua. Alipewa Kiriati-Arba au muji wa Arba ambaye alikuwa babu wa Anaki. Muji huo sasa unaitwa Hebroni. Kalebu alizifukuza kutoka muji huo ukoo tatu za Anaki, ni kusema ukoo wa Sesayi, ukoo wa Ahimani na ukoo wa Talmayi. Kutoka Hebroni alikwenda kuwashambulia wakaaji wa Debiri, muji ambao zamani uliitwa Kiriati-Seferi. Kalebu akatangaza kwamba atamwoesha binti yake Akisa kwa mwanaume yeyote atakayeuteka muji wa Kiriati-Seferi. Basi, Otinieli mwana wa Kenazi, ndugu ya Kalebu, akauteka muji huo, naye Kalebu akamupa binti yake. Katika siku yao ya arusi, Akisa akamwambia Otinieli amwombe Kalebu shamba. Akisa alikuwa amepanda juu ya punda, na alipokuwa anashuka chini, Kalebu akamwuliza: “Unataka nikupe nini?” Akisa akamujibu: “Unipe zawadi. Unipe sehemu yenye maji kwa sababu kule Negebu ulikonipa ni jangwa.” Basi, Kalebu akamupa chemichemi za maji zilizokuwa upande wa juu na chini. Lakini watu wa Yuda hawakuweza kuwafukuza Wayebusi, ambao ndio waliokuwa wenyeji wa Yerusalema, na mpaka leo Wayebusi wangali wanaishi katika muji ule pamoja na watu wa Yuda. Sehemu wazao wa Yosefu waliyogawanyiwa kwa kura ilianzia karibu na muto Yordani, upande wa mashariki wa chemichemi ya Yeriko, na kupitia katika jangwa, hata kwenye sehemu za milima mpaka Beteli. Kutoka Beteli, mupaka ulielekea Luzi ukapita Ataroti ambako Waarki waliishi. Kisha ukashuka upande wa magaribi katika inchi ya Wayefeleti hata Beti-Horoni ya Chini na Gezeri na kuishia kwenye bahari ya Mediteranea. Wazao wa Yosefu, ni kusema kabila la Manase na kabila la Efuraimu, walipewa inchi hiyo kuwa urizi wao. Watu wa kabila la Efuraimu kulingana na jamaa zao walipata sehemu yao ambayo mupaka wake upande wa mashariki ulipita Ataroti-Adari hata Beti-Horoni ya Juu, na kuishia bahari ya Mediteranea. Kwa upande wa kaskazini mupaka ulipita Mikimetati na kwa mashariki yake ulizunguka na kuelekea Tanati-Shilo ambako ulipita upande wa mashariki hata Yanoa. Kutoka Yanoa ulikwenda hata Ataroti na Nara, hata kufika Yeriko, ambako uliishia katika muto Yordani. Kutoka Tapua, mupaka ulikwenda upande wa magaribi hata kijito cha Kana na kuishia bahari ya Mediteranea. Hii ndiyo inchi watu wa kabila la Efuraimu waliyopewa kulingana na jamaa zao, pamoja na miji na vijiji ambavyo waliongezewa kutoka kwenye inchi ya kabila la Manase. Waefuraimu hawakuwafukuza Wakanana walioishi Gezeri. Wakanana hao waliendelea kukaa kati ya watu wa Efuraimu mpaka leo, wakiwa watumwa wa kuwafanyia kazi za kulazimishwa. Watu wa kabila la Manase ambaye alikuwa muzaliwa wa kwanza wa Yosefu, vilevile walipewa eneo lao kwa kura. Makiri, muzaliwa wa kwanza wa Manase baba ya Gileadi, alikwisha kupewa kwa kura miji ya Gileadi na Basani, maana alikuwa hodari katika vita. Wengine waliobaki wa kabila la Manase walipewa sehemu yao kwa kura kulingana na ukoo zao. Ukoo hizo zilikuwa zile za Abiezeri, Heleki, Asirieli, Sekemu, Heferi na Semida ambao wote walikuwa wazao wa kiume wa Manase mwana wa Yosefu. Lakini Zelofehadi mwana wa Heferi, mujukuu wa Gileadi mwana wa Makiri mwana wa Manase, hakukuwa na watoto wa kiume, lakini alikuwa na wabinti tu nao walikuwa: Mala, Noa, Hogla, Milka na Tirza. Wabinti hao wakamwendea kuhani Eleazari na Yoshua mwana wa Nuni, na viongozi wengine wakawaambia: “Yawe alimwamuru Musa atugawanyie na sisi wote inchi kama vile wanaume wa kabila letu wanavyogawanyiwa.” Basi kufuatana na amri ya Yawe, Yoshua akawapatia sehemu yao kama alivyowapa wanaume wa kabila lao. Kwa hiyo kabila la Manase liliongezewa sehemu mbili zaidi, ni kusema inchi ya Gileadi na Basani inayokuwa upande mwingine wa muto Yordani, kwa sababu wabinti wa Manase waligawanyiwa sehemu zao kama vile wanaume wa kabila lao walivyogawanyiwa. (Wazao wengine wa Manase walipewa inchi ya Gileadi.) Eneo la kabila la Manase lilianzia Aseri na kwenda hata Mikimetati upande wa mashariki ya Sekemu; halafu mupaka wao ukaendelea upande wa kusini mpaka kwenye inchi ya wakaaji wa Eni-Tapua. Inchi ya Tapua ilikuwa mali ya Manase, lakini muji wa Tapua, ambao ulikuwa kwenye mupaka, ulikuwa mali ya wazao wa Efuraimu. Mupaka huo uliendelea mpaka kwenye kijito cha Kana. Miji iliyokuwa upande wa kusini ya Kana ilikuwa ya Waefuraimu hata ingawa ilikuwa katika inchi ya kabila la Manase. Halafu mupaka ukapita upande wa kaskazini ya kijito Kana na kuishia katika bahari ya Mediteranea. Eneo la kusini lilikuwa la kabila la Efuraimu na eneo la kaskazini lilikuwa la kabila la Manase, mupaka wake ukiwa bahari ya Mediteranea kwa upande wa magaribi. Kabila la Aseri lilikuwa upande wa kaskazini-magaribi wa eneo la Manase na la kaskazini-mashariki lilikuwa kabila la Isakari. Vilevile katika inchi ya kabila la Isakari na kabila la Aseri, kabila la Manase lilipatiwa miji ya Beti-Seani na Ibuleamu pamoja na vijiji vyake, na miji ya Dori, Eni-Dori, Tanaki na Megido pamoja na wakaaji na vijiji vyake; na sehemu moja ya tatu ya Nafati. Lakini wazao wa Manase hawakuweza kuwafukuza wakaaji wa miji hiyo. Wakanana wakaendelea kuishi humo, ingawa hata nyuma ya Waisraeli kuwa na nguvu zaidi, hawakuweza kuwafukuza, lakini tu waliwafanyisha kazi za kulazimishwa. Watu wa kabila la Yosefu walimwendea Yoshua, wakamwambia: “Kwa nini umetugawanyia sehemu moja tu ya inchi sisi ambao Yawe ametubariki hata akatufanya tukuwe wengi sana?” Yoshua akawajibu: “Kama mumekuwa wengi hivyo, hata inchi ya milima ya Efuraimu haiwatoshi tena, basi muende katika pori katika inchi ya Waperizi na ya Warefaimu, mufyeke pori hiyo na kufanya makao yenu kule.” Nao wakamujibu: “Ni kweli kwamba inchi hii ya milima haitutoshi. Hata hivyo wale Wakanana wote wanaokaa kwenye bonde wana magari ya chuma, vilevile wale wote wanaokaa Beti-Seani pamoja na vijiji vyake, na wale wanaoishi katika Bonde la Yezereheli.” Basi, Yoshua akawaambia wazao wa Yosefu, ni kusema kabila la Efuraimu na Manase: “Kweli ninyi mumekuwa wengi na wenye uwezo mukubwa. Haifai mupate sehemu moja tu, lakini tena inchi ya milima itakuwa yenu. Ingawa sasa ni pori, mutaifyeka na kuirizi yote toka upande huu mpaka upande mwingine. Mutawaondoa Wakanana, hata kama wana magari ya chuma na ni wenye nguvu.” Nyuma ya kuishinda ile inchi, Waisraeli wote pamoja wakakusanyika kule Shilo na kulisimika hema la kusanyiko. Kulikuwa kunabaki kati yao makabila saba ambayo hayakuwa yamegawanyiwa sehemu yao ya inchi. Kwa hiyo, Yoshua akawaambia Waisraeli: “Mutangojea mpaka wakati gani kwenda kuikamata inchi ile ambayo Yawe, Mungu wa babu zenu, amewapatia? Muchague watu watatu kutoka kila kabila niwatume katika inchi yote wachunguze na kuchapa taswira kulingana na makabila yao, kisha waniletee habari. Nao wataigawanya inchi hiyo kwa sehemu saba. Kabila la Yuda litabaki na sehemu yake ya kusini na kabila la Yosefu kaskazini. Mutayarishe maelezo kamili juu ya sehemu zote saba na kuniletea. Hapo, nitapiga kura mbele ya Yawe, Mungu wetu, juu ya sehemu ya kila kabila lenu. Lakini Walawi hawatapata sehemu yoyote kati yenu, maana sehemu yao ni kuwa makuhani wa kumutumikia Yawe. Gadi, Rubeni na nusu ya kabila la Manase walikwisha kupata sehemu yao upande wa mashariki wa muto Yordani. Walipewa sehemu hii na Musa, mutumishi wa Yawe.” Basi, watu hao wakaanza safari ya kwenda kuichunguza inchi. Mbele hawajakwenda, Yoshua akawapa maagizo: “Muende katika inchi yote muandike maelezo kamili juu ya hiyo inchi, kisha murudie kunielezea, nami nitapiga kura mbele ya Yawe hapahapa Shilo juu ya sehemu mutakayopewa.” Wanaume hao wakazunguka katika inchi yote, wakachapa taswira kamili juu ya sehemu zake saba pamoja na miji yake, kisha wakarudi kwa Yoshua kule katika kambi Shilo. Kule Shilo, Yoshua akazipigia kura sehemu hizo mbele ya Yawe, akawagawanyia Waisraeli; kila kabila na sehemu yake. Kura ya kwanza ililipata kabila la Benjamina kulingana na ukoo zake. Eneo walilopewa watu hao lilikuwa katikati ya lile la kabila la Yuda na lile la kabila la Yosefu. Mupaka wake wa kaskazini ulianzia kwenye muto Yordani na kupitia upande wa kaskazini wa Yeriko na inchi ya milima ukaelekea upande wa magaribi mpaka kwenye jangwa la Beti-Aweni. Kutoka kule, mupaka wake ulikwenda kusini kuelekea Luzi kupitia upande wa kusini wa Luzi, ni kusema Beteli, hata Ataroti-Adari, kwenye mulima unaokuwa upande wa kusini wa Beti-Horoni ya Chini. Upande wa magaribi wa mulima huo unaokuwa upande wa kusini wa Beti-Horoni, mupaka uligeuka ukaelekea kusini hata Kiriati-Bali, muji unaoitwa vilevile Kiriati-Yearimu, muji ambao ni mali ya kabila la Yuda. Huu ndio uliokuwa mupaka wake upande wa magaribi. Upande wa kusini mupaka wake ulianzia Kiriati-Yearimu, ukafika Efuroni na kwenda mpaka kwenye chemichemi ya maji ya Nefutoa. Kisha ulielekea chini kupitia pembeni ya mulima unaokuwa karibu na bonde la mwana wa Hinomu, ambalo lilikuwa katika sehemu ya kaskazini zaidi ya bonde la Warefaimu. Halafu mupaka uliteremuka kuelekea bonde la Hinomu, upande wa kusini wa kilima cha Wayebusi, ukaendelea kuteremuka mpaka Eni-Rogeli. Kule, mupaka uligeuka kwenda kaskazini kuelekea Eni-Semesi, ukapitia Geliloti karibu na mwinuko wa Adumimu na kuteremuka mpaka kwenye jiwe la Bohani mwana wa Rubeni. Kutoka pale, mupaka ulizunguka upande wa kaskazini kwenye ukingo wa juu wa Araba na kuishia kule Araba. Tena, ukaendelea kwa upande wa kaskazini wa kilima cha Beti-Hogla na kuishia kaskazini kabisa ya guba ya bahari ya Chumvi, pahali muto Yordani unapoingilia. Huu ni mupaka wake kwa upande wa kusini. Muto Yordani ndio uliokuwa mupaka wake upande wa mashariki. Ndivyo zilivyowekewa mipaka inchi zilizopewa ukoo za kabila la Benjamina. Kura ya pili ilizipata ukoo za kabila la Simeoni na sehemu yao ya inchi ilikuwa imezungukwa na ile ya kabila la Yuda. Kwa vile eneo lililopewa kabila la Yuda lilikuwa kubwa kuliko kabila hilo lilivyohitaji, sehemu ya eneo lake lilipewa kabila la Simeoni. Kura ya tatu ilizipata ukoo za kabila la Zebuluni. Eneo lao lilienea mpaka Saridi. Kutokea kule mupaka wake ulikwenda upande wa magaribi hata Marali, ukapitia pembeni ya Dabeseti na kwenda kwenye kijito kinachokuwa upande wa mashariki wa Yokinamu. Kutokea Saridi, mupaka ule ulielekea mashariki hata kwenye mupaka wa Kisiloti-Tabori, na kutokea kule ukapita Daberati mpaka Yafia. Kutokea Yafia uliendelea upande wa mashariki hata Gati-Heferi, Eti-Kasini, na kuendelea mpaka Rimoni ambako ulipanda kuelekea Nea. Upande wa kaskazini mupaka uligeuka kuelekea Hanatoni na kuishia kwenye bonde la Ifitaheli. Ukakusanya miji ya Katati, Nahalali, Simuroni, Idala na Betelehemu. Jumla ya miji waliyopewa ni kumi na miwili pamoja na vijiji vyake. Hiyo ndiyo sehemu zilizopewa ukoo za kabila la Zebuluni miji hiyo pamoja na vijiji vyake. Kura ya ine ilizipata ukoo za kabila la Isakari. Hiyo ndiyo sehemu zilizopewa ukoo za kabila la Isakari; miji hiyo pamoja na vijiji vyake. Kura ya tano ilizipata ukoo za kabila la Aseri. Eneo la inchi yao lilikuwa na miji ya: Helkati, Hali, Beteni, Akisafu, Alameleki, Amadi na Misali. Kwa upande wa magaribi mupaka uligusana na Karmeli na Sihori-Libunati. Kisha ukageuka kuelekea mashariki kwenda Beti-Dagoni ambako unagusana na Zebuluni na bonde la Ifitaheli. Halafu ukaendelea kaskazini ukafika Beti-Emeki, Neieli na kuzidi kuelekea kaskazini ukafika Kabuli, Eburoni, Rehobu, Hamoni, Kana mpaka Sidona muji mukubwa. Hapo, mupaka uligeuka kuelekea Rama na kufikia kwenye muji wa Tiro uliokuwa na kuta. Kisha ukageuka kuelekea Hosa na kuishia kwenye bahari ya Mediteranea. Miji mingine iliyokuwa katika eneo lile ni Maharabu, Akizibu, Uma, Afeki na Rehobu. Jumla ya miji waliyopewa ni makumi mbili na mbili pamoja na vijiji vyake. Hiyo ndiyo sehemu zilizopewa ukoo za kabila la Aseri; miji hiyo pamoja na vijiji vyake. Kura ya sita ilizipata ukoo za kabila la Nafutali. Mupaka wake ulianzia Helefi na kwenye muti wa mwalo wa Zananimu, ukapita Adami-Nekebu na Yabuneli ukafika Lakumu na kuishia kwenye muto Yordani. Kutoka pale mupaka ulikwenda upande wa magaribi kuelekea Asinoti-Tabori; tokea kule ukaenda Hukoki na kugusana na pembe ya kusini ya eneo la kabila la Zebuluni; kisha kugusana na eneo la kabila la Aseri upande wa magaribi, na kugusana na eneo la kabila la Yuda. Kwa upande wa mashariki mupaka uliingilia kwenye muto Yordani. Hiyo ndiyo sehemu zilizopewa ukoo za kabila la Nafutali; miji hiyo pamoja na vijiji vyake. Kura ya saba ilizipata ukoo za kabila la Dani. Watu wa kabila la Dani walipopoteza inchi yao, walikwenda na kuushambulia muji wa Lesemu. Waliushinda na kuuteka, na nyuma ya kuwaua wakaaji wake wote, wakaurizi halafu wakabadilisha jina la muji ule kuwa Dani; jina ambalo lilikuwa ni la babu yao. Hiyo ndiyo sehemu zilizopewa ukoo za kabila la Dani; miji hiyo pamoja na vijiji vyake. Walipomaliza kugawanyana sehemu zote za inchi, Waisraeli walimupa Yoshua mwana wa Nuni, sehemu yake katikati yao. Kulingana na amri ya Yawe walimupa muji ambao aliuchagua yeye mwenyewe, ni kusema Timunati-Sera, ambao ulikuwa katika inchi ya milima ya Efuraimu. Naye Yoshua akaujenga upya muji ule na kukaa mule. Basi, kuhani Eleazari na Yoshua mwana wa Nuni, pamoja na viongozi wa makabila ya Waisraeli waligawanya sehemu hizo kwa kura mbele ya Yawe kwenye mulango wa hema ya kusanyiko kule Shilo. Basi, wakakamilisha kuigawanya inchi. Kisha Yawe akamwambia Yoshua, awaambie Waisraeli hivi: “Mujichagulie miji ambamo mutu anaweza kukimbilia usalama ambayo nilimwambia Musa akuelezee. Mutu yeyote akimwua mutu bila kukusudia anaweza kukimbilia katika muji mumoja na hivyo anaweza kuepuka yule mutu anayekuwa na ruhusa ya kulipiza kisasi cha damu. Mwuaji atakimbilia katika muji mumoja wa miji ile na kusimama kwenye mulango wa muji na kuwaelezea wazee wa muji ule maneno yake. Wazee watamupokea ndani na kumupa pahali pa kuishi pamoja nao. Kama yule mutu mwenye kuwa na ruhusa ya kulipiza kisasi akimufuatilia mpaka katika muji ule, wazee wa muji ule hawaruhusiwi kumutoa mwuaji yule kwa yule mwenye kutaka kulipiza kisasi maana alimwua mwenzake kwa bahati mbaya tu kwa vile hakukukuwa uadui kati yao zamani. Mwuaji ataendelea kuishi mule mpaka pale atakapohukumiwa mbele ya mukutano wote wa Waisraeli na vilevile mpaka pale yule Kuhani Mukubwa ambaye alikuwa na madaraka wakati ule atakapokufa. Nyuma ya pale mutu huyo ataweza kurudi katika nyumba yake katika muji ule pahali alipotoka wakati alipotoroka.” Basi, kwa ajili hiyo wakaitenga miji ya Kedesi katika Galilaya kwenye milima ya Nafutali, Sekemu katika milima ya Efuraimu na Kiriati-Arba, ni kusema Hebroni, katika inchi ya milima ya Yuda. Na ngambo ya muto Yordani, upande wa mashariki wa muji wa Yeriko, walichagua muji wa Bezeri unaokuwa kwenye jangwa katika mabonde ya eneo la kabila la Rubeni. Vilevile wakachagua Ramoti, kule Gileadi ambao ni muji wa kabila la Gadi na Golani kule Basani katika eneo la kabila la Manase. Hii ndiyo miji iliyotengwa kwa ajili ya watu wote wa Israeli na wageni walioishi kati yao, kusudi mutu yeyote atakayemwua mwenzake bila kukusudia akimbilie kule asipate kuuawa na mwenye ruhusa ya kulipiza kisasi cha damu, mpaka pale atakapohukumiwa mbele ya mukutano wa watu wote. Walipokuwa kule Shilo katika inchi ya Kanana viongozi wa ukoo za Walawi wakawaendea kuhani Eleazari na Yoshua mwana wa Nuni, na viongozi wa jamaa za makabila yote ya Waisraeli, wakawaambia: “Yawe alimwagiza Musa kwamba tupewe miji ya kuishi na mbuga za malisho ya nyama wetu.” Basi, kulingana na amri ya Yawe, Waisraeli walichagua kutoka katika maeneo ya inchi zao, miji na vijiji vya malisho, wakawapa Walawi ikuwe sehemu yao. Kura ya kwanza ilizipata jamaa za ukoo wa Kohati. Kati ya wazao wa kuhani Haruni walipewa kwa kura, miji iliyokuwa katika maeneo ya makabila ya Yuda, Simeoni, na Benjamina. Jumla ya miji waliyopewa ni kumi na mitatu. Watu wa ukoo wa Kohati waliobaki wakapewa miji kumi inayokuwa katika maeneo ya makabila ya Efuraimu, Dani na katika eneo la nusu ya kabila la Manase. Watu wa ukoo wa Gersoni wakapewa kwa kura miji kumi na mitatu katika maeneo ya makabila ya Isakari, Aseri, Nafutali na katika eneo la nusu ya kabila la Manase kule Basani. Jamaa za ukoo wa Merari wakapewa miji kumi na miwili katika maeneo ya makabila ya Rubeni, Gadi na Zebuluni. Waisraeli wakawapa Walawi miji hiyo pamoja na vijiji vya malisho yao, kama Yawe alivyomwagiza Musa. Haya ndiyo majina ya miji kutoka kwenye maeneo ya kabila la Yuda na Simeoni ambayo ilitolewa kwa wazao wa kuhani Haruni, waliokuwa jamaa za ukoo wa Kohati ambaye alikuwa wa kabila la Lawi. Sehemu yao walipata kwanza maana kura yao ilitokea kwanza. Wakapewa Kiriati-Arba, ni kusema Hebroni (Arba alikuwa baba ya Anaki), katika milima ya Yuda, pamoja na mbuga zilizoizunguka. Lakini mashamba ya muji ule pamoja na vijiji vilivyouzunguka vilikuwa vimekwisha kupewa kwa Kalebu mwana wa Yefune vikuwe mali yake. Zaidi ya kuwapa wazao wa kuhani Haruni muji wa Hebroni ambao vilevile ulikuwa umetengwa kuwa muji wa kukimbilia usalama, waliwapa miji ya Libuna pamoja na mbuga zake za malisho; Yatiri pamoja na mbuga zake za malisho, Estemoa pamoja na mbuga zake za malisho, Holoni pamoja na mbuga zake za malisho, Debiri pamoja na mbuga zake za malisho. Aini pamoja na mbuga zake za malisho, Yuta pamoja na mbuga zake za malisho na Beti-Semesi pamoja na mbuga zake za malisho. Jumla ya miji hiyo inayokuwa katika maeneo ya makabila hayo mawili ni tisa. Katika eneo la kabila la Benjamina walipewa miji mingine: Gibeoni pamoja na mbuga zake za malisho, Anatoti pamoja na mbuga zake za malisho, Almoni pamoja na mbuga zake za malisho. Jumla ya miji waliyopewa ni mine. Miji yote ya wazao wa Haruni ambao walikuwa makuhani, ilikuwa kumi na mitatu pamoja na mbuga zao za malisho. Watu waliobaki wa ukoo wa Kohati, ambao vilevile ni watu wa ukoo wa Lawi walipewa miji katika eneo la kabila la Efuraimu. Walipewa Sekemu, muji ambao ulikuwa vilevile muji wa kukimbilia usalama, pamoja na mbuga zake za malisho katika inchi ya milima ya Efuraimu, na Gezeri pamoja na mbuga zake za malisho, Kibusaimu pamoja na mbuga zake za malisho na Beti-Horoni pamoja na mbuga zake za malisho. Jumla ya miji waliyopewa ni mine. Katika eneo la kabila la Dani walipewa Elteke pamoja na mbuga zake za malisho, Gibetoni pamoja na mbuga zake za malisho, Ayaloni pamoja na mbuga zake za malisho, na Gati-Rimoni pamoja na mbuga zake za malisho. Jumla ya miji waliyopewa ni mine. Katika eneo la nusu ya kabila la Manase walipewa Tanaki pamoja na mbuga zake za malisho na Gati-Rimoni pamoja na malisho yake. Jumla ya miji waliyopewa ni miwili. Basi, miji ambayo walipewa watu wa ukoo wa Kohati iliyobaki ilikuwa kumi pamoja na mbuga zao za malisho. Watu wa uzao wa Lawi wa ukoo wa Gersoni, walipewa miji miwili katika nusu ya eneo la kabila la Manase: Golani, kule Basani, muji wa kukimbilia usalama, pamoja na mbuga zake za malisho, na Be-Estera pamoja na malisho yake. Katika eneo la kabila la Isakari, walipewa Kisioni pamoja na mbuga zake za malisho, Daberati pamoja na mbuga zake za malisho, Yarmuti pamoja na mbuga zake za malisho na Eni-Ganimu pamoja na mbuga zake za malisho. Jumla ya miji waliyopewa ni mine. Katika eneo la kabila la Aseri walipewa Misali pamoja na mbuga zake za malisho, Abudoni pamoja na mbuga zake za malisho, Helkati pamoja na mbuga zake za malisho na Rehobu pamoja na mbuga zake za malisho. Jumla ya miji waliyopewa ni mine. Katika eneo la kabila la Nafutali walipewa Kedesi, muji wa kukimbilia usalama unaokuwa kule Galilaya pamoja na mbuga zake za malisho, Hamoti-Dori pamoja na mbuga zake za malisho na Kartani pamoja na mbuga zake za malisho. Kwa jumla, miji mitatu. Jumla ya miji ya jamaa mbalimbali za ukoo wa Gersoni ilikuwa kumi na mitatu pamoja na mbuga zao za malisho. Walawi wengine waliobaki, ni kusema wazao wa Merari, walipewa miji katika eneo la kabila la Zebuluni. Nayo ni Yokinamu pamoja na mbuga zake za malisho, Karta pamoja na mbuga zake za malisho, Dimuna pamoja na mbuga zake za malisho na Nahalali pamoja na mbuga zake za malisho. Kwa jumla, miji mine. Katika eneo la kabila la Rubeni walipewa Bezeri pamoja na mbuga zake za malisho, Yahazi pamoja na mbuga zake za malisho, Kedemoti pamoja na mbuga zake za malisho na Mefati pamoja na mbuga zake za malisho. Kwa jumla, miji mine. Katika eneo la kabila la Gadi walipewa Ramoti wa Gileadi, muji wa kukimbilia usalama, pamoja na mbuga zake za malisho, Mahanaimu pamoja na mbuga zake za malisho, Hesiboni pamoja na mbuga zake za malisho na Yazeri pamoja na mbuga zake za malisho. Jumla miji mine. Miji yote waliyopewa wazao wa Merari, ni kusema watu wa ukoo wa Walawi zilizobaki, ilikuwa kumi na miwili. Jumla ya miji yote ambayo Walawi walipewa katika maeneo ya Waisraeli ilikuwa makumi ine na nane pamoja na mbuga zao za malisho. Kila mumoja kati ya miji hii ulizungukwa na mbuga za malisho. Basi, Yawe aliwapa Waisraeli inchi yote ambayo alikuwa amewaahidi wazee wao. Nao wakairizi na kuishi mule. Yawe akawapa amani kila pahali katika inchi kama vile alivyowaapia wazee wao. Hakuna adui yeyote aliyesubutu kuwashambulia maana Yawe alikuwa amewatia waadui hao katika mikono yao. Hakuna hata ahadi yoyote njema ambayo Yawe aliiahidi Waisraeli ambayo haikutimia. Ahadi zote zilitimia. Basi, Yoshua akawaita watu wa kabila la Rubeni, la Gadi na watu wa nusu ya kabila la Manase akawaambia: “Ninyi mumefuata yale yote Musa, mutumishi wa Yawe, aliyowaamuru na mumetii maagizo niliyowaamuru. Wala hamukuwaacha wandugu zenu kwa muda ule wote murefu mpaka leo, lakini mumefuata kwa uangalifu amri ya Yawe, Mungu wenu. Sasa Yawe, Mungu wenu, amewapa wandugu zenu amani, kama vile alivyoahidi, basi, murudie kwenu katika inchi ambayo mulipewa na Musa mutumishi wa Yawe, ikuwe mali yenu, ni kusema ngambo ya muto Yordani. Mukuwe waangalifu kutii amri na sheria ambazo Musa, mutumishi wa Yawe, aliwaamuru: mumupende Yawe, Mungu wenu, mufuate anachotaka na kushika amri zake, mukae pamoja naye na kumutumikia kwa moyo wote na roho yote.” Basi, Yoshua akawabariki na kuwaruhusu waende zao akawaambia: Basi, watu wa Rubeni, Gadi na nusu ya kabila la Manase wakaachana na watu wa makabila mengine ya Israeli kule Shilo katika inchi ya Kanana, wakarudi kwao katika inchi ya Gileadi, inchi yao wenyewe walioirizi kwa amri ya Yawe kama vile alivyomwagiza Musa. Walipofika kwenye muto Yordani wakiwa bado katika inchi ya Kanana, wakajenga mazabahu kubwa sana karibu na muto huo. Basi, habari zikawafikia watu wa makabila mengine ya Israeli kwamba makabila ya Rubeni, Gadi na nusu ya kabila la Manase yalikuwa yamejenga mazabahu kubwa karibu na muto Yordani katika inchi ya Kanana, ni kusema ndani ya eneo lao. Waliposikia hivyo, Waisraeli walikusanyika wote kule Shilo kwenda kupigana vita na hayo makabila ya upande wa mashariki. Basi, watu wa Israeli wakamutuma Finehasi mwana wa kuhani Eleazari, kule Gileadi kwa makabila ya Rubeni, Gadi na nusu ya kabila la Manase. Finehasi akaondoka pamoja na wakubwa kumi, kila mumoja akiwa mukubwa wa jamaa katika kabila lake. Nao wakawaendea watu wa makabila ya Rubeni, Gadi na nusu ya kabila la Manase kule Gileadi wakawaambia: “Watu wote wa Yawe wanauliza hivi: ‘Ni udanganyifu gani huu mumemufanyia Mungu wa Israeli? Mbona mumemwasi Yawe kwa kujenga mazabahu hii? Zambi tulizotenda kule Peori hazitoshi? Hamwoni kwamba bado hatujajitakasa na kwamba mateso yake bado yanaisumbua watu wa Yawe? Kwa nini, basi, mumeacha kumufuata Yawe? Mukimwasi Yawe leo, kesho atakasirikia sana Waisraeli wote pamoja. Basi, ikiwa inchi yenu muliorizi ni chafu, mukuje katika inchi ya Yawe ambako hema yake iko na kujitwalia sehemu kule pamoja nasi; lakini tu musimwasi Yawe na kutufanya sisi wote waasi kwa kujijengea ninyi wenyewe mazabahu isiyokuwa ya Yawe, Mungu wetu. Akana mwana wa Zera alipokosa uaminifu katika vitu vitakatifu, kasirani haikuangukia Waisraeli wote pamoja? Tena Akana hakukufa tu yeye peke yake kwa sababu ya uovu wake.’ ” Hapo watu wa makabila ya Rubeni na Gadi na nusu ya kabila la Manase wakawajibu viongozi wa jamaa za Waisraeli: “Mungu wa miungu ndiye Yawe! Mungu wa miungu ndiye Yawe! Yeye anajua kwa nini tumefanya hivyo. Na Waisraeli wote watajua vilevile! Kama huu ni uasi au ni ukosefu wa imani kwa Yawe basi, yeye aache kutuokoa leo. Kama tumemwacha Yawe tukajenga mazabahu yetu wenyewe kusudi tutoe sadaka za kuteketezwa kwa moto, za unga au za amani, basi Yawe atulipize kisasi. Lakini sivyo inavyokuwa. Tuliijenga kwa kuogopa kwamba labda katika siku zinazokuja watoto wenu watawaambia watoto wetu: ‘Ninyi muko na uhusiano gani na Yawe, Mungu wa Israeli? Hamwoni kwamba Yawe ameweka muto wa Yordani kuwa mupaka kati yenu na sisi? Ninyi makabila ya Rubeni na kabila la Gadi hamuna fungu lolote lenu kwa Yawe.’ Hivyo watoto wenu wangeweza kisha kusababisha watoto wetu waache kumwabudu Yawe. Ndiyo maana tuliamua kujenga mazabahu hii, lakini si kwa ajili ya kutolea juu yake sadaka za kuteketezwa kwa moto wala sadaka zingine, lakini tulitaka mazabahu hii ikuwe ushuhuda kati yetu na ninyi na vizazi vyetu vinavyokuja kwamba sisi tuna haki ya kumutumikia Yawe kwa sadaka zetu za kuteketezwa kwa moto na sadaka zetu zingine, na kwa sadaka zetu za amani, kusudi watoto wenu wasipate kuwaambia watoto wetu kwamba hawana fungu lolote lao kwa Yawe. Tena tulifikiri kwamba ikiwa jambo kama hilo litasemwa juu yetu au juu ya wazao wetu katika siku zinazokuja, tutasema: ‘Muangalie mufano wa mazabahu ya Yawe ambayo wazee wetu waliijenga; sio kwa ajili ya kutolea juu yake sadaka za kuteketezwa kwa moto au sadaka zingine lakini kama ushuhuda kati yetu na ninyi’. Sisi hatukuwa na nia ya kumwasi sasa Yawe hata kidogo na kumwacha kwa kujenga mazabahu ya kutolea sadaka za kuteketezwa kwa moto au sadaka za unga au sadaka zingine. Hatupendi kutolea sadaka pahali pengine isipokuwa juu ya mazabahu ya Yawe, Mungu wetu, inayokuwa katika makao yake.” Kuhani Finehasi na wakubwa wa jamaa za Waisraeli waliokuwa pamoja naye waliposikia maneno hayo ya watu wa makabila ya Rubeni na Gadi na nusu ya kabila la Manase, wakafurahi. Naye Finehasi mwana wa kuhani Eleazari, akayaambia makabila ya Rubeni na Gadi na nusu ya kabila la Manase: “Leo tumejua kwamba Yawe yuko kati yenu maana hamukumufanyia Mungu uasi. Sasa mumewaokoa Waisraeli wasiazibiwe na Yawe.” Basi, Finehasi mwana wa kuhani Eleazari pamoja na viongozi wenzake wakawaaga watu wa makabila ya Rubeni na Gadi wakaondoka katika inchi ya Gileadi, wakarudi Kanana kwa Waisraeli na kuwapa habari hizo. Habari hiyo ikawafurahisha Waisraeli, wakamushukuru Yawe na kuacha mipango yao ya vita na kusudi lao la kuharibu kabisa inchi iliyokuwa ya makabila ya Rubeni na Gadi. Watu wa makabila ya Rubeni na Gadi wakaiita ile mazabahu “Ushuhuda”, maana walisema: “Mazabahu hii ni ushuhuda wetu kwamba Yawe ndiye Mungu.” Nyuma ya muda murefu, Yawe aliwajalia Waisraeli amani kwa kuwaokoa na waadui zao pande zote. Wakati ule Yoshua alikuwa muzee wa miaka mingi. Yoshua aliwaita Waisraeli wote pamoja na viongozi na wazee wao, waamuzi na wakubwa, akawaambia: “Sasa mimi nimekuwa muzee wa miaka mingi. Ninyi mumeona mambo yote Yawe, Mungu wenu, aliyoyatendea mataifa haya yote kwa ajili yenu. Yawe, Mungu wenu, ndiye aliyewapigania. Inchi za mataifa yaliyobaki na yale niliyoyaangamiza nimewagawanyia zikuwe mali ya makabila yenu, kutoka Yordani mpaka bahari ya Mediteranea, upande wa magaribi. Yawe, Mungu wenu, atayaondoa mbele yenu na kuyafukuza kabisa, nanyi mutarizi inchi yao kama vile Yawe, Mungu wenu, alivyowaahidi. Kwa hiyo, mukuwe imara katika kushika yote yaliyoandikwa katika kitabu cha Sheria ya Musa, musiyaache hata kidogo. Musishirikiane na mataifa haya yaliyobaki kati yenu. Musiitaje miungu yao wala musiape kwa majina ya miungu yao; musiitumikie wala kuinama mbele yao. Lakini muambatane na Yawe, Mungu wenu, kama mulivyofanya mpaka leo. Maana Yawe ameyafukuza mbele yenu mataifa makubwa na yenye nguvu na hakuna mutu ambaye ameweza kuwapinga ninyi mpaka leo. Mutu wenu mumoja tu anaweza kuwakimbiza waadui elfu moja, maana Yawe Mungu wenu ndiye anayewapigania kama alivyowaahidi. Basi, mukuwe waangalifu sana kumupenda Yawe, Mungu wenu. Maana, kama mukimwasi Yawe na kujiunga na mataifa haya yaliyobaki kati yenu, mukioa kwao nao wakioa kwenu, mujue kwa hakika kwamba Yawe, Mungu wenu, hataendelea kuyafukuza mataifa haya mbele yenu, lakini yatakuwa kwenu kikwazo na mutego. Yatakuwa kwenu mujeledi wa kuwapiga na miiba ya kuwachoma kwa macho mpaka pale mutakapoangamia na kutoka katika inchi hii nzuri ambayo Yawe, Mungu wenu, amewapa. “Sasa, wakati wangu wa kufa kama inavyokuwa kawaida ya wanadamu wote umekaribia. Lakini ninyi wote munajua wazi ndani ya mioyo na roho zenu kwamba katika mambo yote mema ambayo Yawe, Mungu wenu aliwaahidi, hakuna hata moja ambalo halikutimia. Yote yametimia kama vile alivyoahidi. Lakini kama vile Yawe, Mungu wenu, alivyotimiza mambo yote mema aliyowaahidi, ni vile vile anavyoweza kuwaletea maovu yote mpaka awaangamize wote kutoka inchi hii nzuri ambayo amewapa. Kama mukivunja agano la Yawe, Mungu wenu, ambalo aliwaamuru mulishike, mukienda kuitumikia miungu mingine na kuinama mbele yao; basi, hasira ya Yawe itawaka juu yenu, nanyi mutaangamia mara moja kutoka inchi hii nzuri ambayo amewapa.” Kisha Yoshua akayakusanya makabila yote ya Waisraeli kule Sekemu. Akawaita wazee, viongozi, waamuzi na wakubwa wa Waisraeli, nao wakakuja mbele ya Mungu. Yoshua akawaambia watu wote: “Yawe, Mungu wa Israeli, anasema hivi: Hapo zamani, wazee wenu waliishi ngambo ya muto Furati, wakaitumikia miungu mingine. Muzee mumoja aliitwa Tera, baba ya Abrahamu na Nahori. Mimi Mungu nilimwondoa babu yenu Abrahamu kutoka kule ngambo ya muto Furati na kumuleta hapa Kanana, ambako nilimupatia wazao wengi. Nilimupa Isaka, naye Isaka nikamupa Yakobo na Esau. Nilimupa Esau milima ya Seiri airizi. Lakini Yakobo na watoto wake walikwenda Misri. Nyuma nikawatuma Musa na Haruni, nikailetea inchi ya Misri mapigo, na kisha nikawatoa ninyi katika inchi ile. Niliwatoa wazee wenu kutoka Misri na kuwaleta mpaka kwenye bahari Nyekundu. Wamisri waliwafuatilia wakiwa na magari na waaskari wapanda-farasi. Waisraeli waliponililia mimi Yawe, niliweka giza kati yao na Wamisri na kuifanya bahari iwafunike Wamisri. Ninyi wenyewe mulijionea yale niliyowatendea Wamisri. Muliishi katika jangwa muda murefu. Kisha niliwaongoza mpaka katika inchi ya Waamori ambao waliishi upande mwingine wa muto Yordani. Walipigana nanyi, lakini mimi niliwapa ushindi juu yao mukawaangamiza na kuiteka inchi yao. Naye Balaka mwana wa Sipori, mufalme wa Moabu, akakuja na kuwashambulia Waisraeli. Akamwalika Balama mwana wa Beori akuje kuwalaani ninyi. Lakini mimi sikumusikiliza Balama, naye akawabariki, nami nikawaokoa ninyi toka mikono ya Balaka. Halafu mukavuka muto Yordani, mukafika Yeriko. Wakaaji wa Yeriko walipigana nanyi, vilevile na Waamori, Waperizi, Wakanana, Wahiti, Wagirgasi, Wahivi na Wayebusi. Hao mimi nikawatia katika mikono yenu. Nilituma nyuki mbele yenu ambazo ziliwafukuza wafalme wawili wa Waamori. Hamukufanya yale kwa kukamata mapanga wala mishale yenu. “Niliwapa mashamba ambayo hamukukuwa mumeyalima, na miji ambayo hamukuijenga ambamo sasa munaishi, na kula matunda ya mizabibu na mizeituni ambayo hamukuipanda. “Sasa, basi, mumutii Yawe na kumutumikia kwa moyo wa haki na uaminifu. Muache kabisa miungu ile ambayo wazee wenu waliiabudu ngambo ya muto Furati na katika inchi ya Misri. Mumutumikie Yawe. Kama hamutaki kumutumikia Yawe, basi muchague leo hii ni nani mutakayemutumikia: kama ni miungu ile ambayo wazee wenu waliitumikia ngambo ya muto Furati, au miungu ya Waamori ambao sasa munaishi katika inchi yao. Lakini mimi na jamaa yangu, tutamutumikia Yawe.” Halafu watu wakamujibu: “Hatutaweza hata kidogo kumwacha Yawe na kuitumikia miungu mingine. Maana, Yawe, Mungu wetu, ndiye aliyetutoa sisi pamoja na wazee wetu katika inchi ya Misri tulikokuwa watumwa, tukayaona kwa macho yetu wenyewe matendo ya ajabu aliyotenda. Akatulinda katika safari zetu zote na kati ya watu wote ambao tulipita kati yao. “Yawe alituondolea watu wote, ni kusema Waamori wote waliokaa katika inchi. Kwa hiyo, nasi tutamutumikia Yawe, maana ndiye Mungu wetu.” Lakini Yoshua akawaambia: “Ninyi hamuwezi kumutumikia Yawe, maana yeye ni Mungu Mutakatifu. Yeye ni Mungu mwenye wivu, naye hatawasamehe makosa na zambi zenu. Mukimwacha Yawe na kuitumikia miungu ya kigeni, atawaazibu na kuwaangamiza ninyi, hata ingawa amewatendea mema haya yote.” Nao watu wakamwambia Yoshua: “Hapana! Sisi tutamutumikia Yawe tu.” Halafu Yoshua akawaambia: “Ninyi ni washuhuda wenu wenyewe kwamba mumechagua kumutumikia Yawe.” Nao wakamujibu: “Sisi ni washuhuda.” Naye akawaambia: “Basi, muondoe miungu ya kigeni munayokuwa nayo, mumufuate Yawe, Mungu wa Israeli, kwa moyo wenu wote.” Nao, wakasema: “Tutamutumikia na kumutii Yawe, Mungu wetu.” Hivyo, Yoshua akafanya agano na Waisraeli kule Sekemu, akawapa masharti na maagizo ya kufuata. Yoshua akayaandika haya yote katika kitabu cha sheria ya Mungu; kisha, akatwaa jiwe kubwa na kulisimika chini ya muti wa mwalo katika hema ya Yawe. Halafu akawaambia watu wote: “Jiwe hili ndilo litakalokuwa ushuhuda kwetu, maana limesikia maneno yote ambayo Yawe ametuambia. Kwa hiyo, litashuhudia juu yenu, kusudi musipate kumwasi Mungu wenu.” Halafu Yoshua akawaruhusu watu waondoke; nao wakaenda kila mumoja kwake. Nyuma ya mambo hayo, Yoshua mwana wa Nuni na mutumishi wa Yawe, akakufa akiwa na umri wa miaka mia moja na kumi. Nao wakamuzika kwenye eneo ambalo alikuwa amegawanyiwa kuwa sehemu yake, kule Timunati-Sera, katika milima ya Efuraimu, upande wa kaskazini wa mulima wa Gasi. Waisraeli walimutumikia Yawe muda wote wa maisha ya Yoshua, na nyuma ya kifo chake, waliendelea kumutumikia kwa muda wa maisha ya wale wazee waliokuwa wameona kwa macho yao mambo yale Yawe aliyowatendea Waisraeli. Mifupa ya Yosefu ambayo Waisraeli walikuwa wameileta kutoka Misri waliizika kule Sekemu katika eneo ambalo Yakobo alikuwa amelinunua kutoka kwa wana wa Hamori, baba ya Sekemu, kwa bei ya vikoroti mia moja vya feza. Eneo lile nalo likakuwa mali yao wazao wa Yosefu. Naye Eleazari mwana wa Haruni, akakufa na kuzikwa Gibea, muji ambao mwana wake Finehasi alikuwa amepewa katika inchi ya milima ya Efuraimu. Nyuma ya kifo cha Yoshua, Waisraeli walimwuliza Yawe: “Ni kabila gani litakwenda kupigana kwanza na Wakanana?” Yawe akawajibu: “Kabila la Yuda litakwenda kupigana nao kwanza, maana nimeitia inchi hiyo katika mikono yao.” Watu wa kabila la Yuda wakawaambia wandugu zao, watu wa kabila la Simeoni: “Mushirikiane nasi tunapokwenda kuitwaa inchi hiyo ambayo tumepewa. Nasi, vilevile tutashirikiana nanyi kwenda kuitwaa inchi mutakayopewa.” Hivyo kabila la Simeoni likakubali kushirikiana nao. Basi watu wa kabila la Yuda wakaenda kufanya mashambulio, naye Yawe akawatia Wakanana na Waperizi katika mikono yao, wakawaua watu elfu kumi katika vita kule Bezeki. Katika muji ule wakamukuta mufalme Adoni-Bezeki, wakapigana naye na kuwashinda Wakanana na Waperizi. Adoni-Bezeki akakimbia, lakini walimufuatilia, wakamukamata, wakamukata vidole gumba vya mikono na miguu. Adoni-Bezeki akasema: “Wafalme makumi saba waliokatwa vidole gumba vya mikono na miguu waliokota makombo chini ya meza yangu. Sasa Mungu amenilipa kama nilivyotenda.” Wakamupeleka Yerusalema, akakufia kule. Watu wa kabila la Yuda waliushambulia Yerusalema na kuuteka. Waliwaua wakaaji wake kwa mapanga na kuuteketeza muji kwa moto. Kisha, watu wa kabila la Yuda wakakwenda kupigana na Wakanana walioishi kwenye inchi ya milima, Negebu na kwenye inchi ya bonde. Waliwashambulia vilevile Wakanana walioishi katika muji wa Hebroni ambao zamani uliitwa Kiriati-Arba, wakashinda makabila ya Sesai, Ahimani na Talmayi. Kutoka kule watu wa kabila la Yuda walikwenda kuushambulia muji wa Debiri; ambao zamani uliitwa Kiriati-Seferi. Kalebu akatangaza: “Mutu yeyote atakayeshinda na kuuteka muji wa Kiriati-Seferi, nitamupa binti yangu Akisa kuwa muke wake.” Basi, Otinieli mwana wa Kenazi na mudogo wa Kalebu, akauteka, naye Kalebu akamutoa binti yake Akisa aolewe na Otinieli. Akisa alipofika kwa Otinieli, akamwambia Otinieli amwombe baba yake Kalebu shamba. Akisa alikuwa amepanda juu ya punda na aliposhuka chini baba yake akamwuliza: “Ungependa nikupe nini?” Akamujibu: “Unipe zawadi! Ninaomba unipe chemichemi za maji maana kule upande wa kusini ni jangwa.” Kalebu akamupa chemichemi za upande wa juu na za chini. Wazao wa Keni ambaye alikuwa baba mukwe wa Musa, walifuatana na watu wa kabila la Yuda kutokea Muji wa Miti ya Ngazi, ni kusema muji wa Yeriko, mpaka jangwa la Yuda karibu na Aradi, wakafanya makao yao kule pamoja na watu wa Yuda. Watu wa kabila la Yuda walishirikiana na wandugu zao, watu wa kabila la Simeoni, wakawashinda Wakanana waliokaa Sefati. Wakaangamiza kabisa muji ule na kugeuza jina lake kuwa Horma, ni kusema “Maangamizo”. Watu wa kabila la Yuda vilevile waliteka miji ya Gaza na eneo lake, Askeloni na eneo lake, na Ekuroni na eneo lake. Yawe alikuwa pamoja na watu wa kabila la Yuda, nao wakaiteka inchi ya milima. Lakini hawakuweza kuwashinda wenyeji wa inchi ya bonde kwa sababu magari yao ya vita yalikuwa ya chuma. Muji wa Hebroni ukapewa kwa Kalebu kufuatana na maagizo ya Musa. Kalebu akazifukuza kutoka kule ukoo tatu za Anaki. Lakini watu wa kabila la Benjamina hawakuwafukuza Wayebusi waliokaa katika Yerusalema; ndiyo maana Wayebusi wanakaa pamoja na watu wa kabila la Benjamina katika Yerusalema mpaka leo. Watu wa makabila ya Yosefu waliushambulia muji wa Beteli, naye Yawe alikuwa pamoja nao. Kwanza walikuwa wamewatuma wapelelezi kwenda kuupeleleza muji wa Beteli. Muji ule zamani uliitwa Luzi. Wapelelezi hao walimwona mutu mumoja akitoka katika muji, wakamwambia: “Tafazali, utuonyeshe njia inayoingia katika muji, nasi tutakutendea mema.” Akawaonyesha njia ya kuingia katika muji. Basi, wakaingia na kuangamiza kila mutu aliyekuwa mule. Lakini wakamwacha salama mutu yule na jamaa yake. Mutu yule akahamia katika inchi ya Wahiti, kule akajenga muji ambao aliuita Luzi, na muji huo unaitwa hivyo mpaka leo. Watu wa kabila la Manase hawakuwafukuza wakaaji wa miji ya Beti-Seani na vijiji vyake, Tanaki na vijiji vyake, Dori na vijiji vyake, Ibileamu na vijiji vyake, na Megido pamoja na vijiji vyake. Wakanana waliendelea kukaa kule. Hata Waisraeli walipokuwa na nguvu hawakuwafukuza Wakanana lakini waliwapa kazi za kulazimishwa. Watu wa kabila la Efuraimu hawakuwafukuza Wakanana walioishi kule Gezeri, na hawa waliishi kule pamoja na watu wa Efuraimu. Watu wa kabila la Zebuluni hawakuwafukuza wakaaji wa muji wa Kitironi, wala wale wa muji wa Nahalali, waliendelea kukaa pamoja nao wakiwatumikisha kazi za kulazimishwa. Watu wa kabila la Aseri hawakuwafukuza wakaaji wa miji ya Ako, Sidona, Alabu, Akizibu, Helba, Afika na Rehobu. Watu wa kabila la Aseri walikaa pamoja na Wakanana wenyeji wa inchi hiyo maana hawakuwafukuza. Watu wa kabila la Nafutali hawakuwafukuza wakaaji wa muji wa Beti-Semesi au wakaaji wa Beti-Anati, lakini walikaa pamoja nao. Hata hivyo wenyeji wa miji hiyo walitumikishwa kazi za kulazimishwa. Waamori waliwafukuzia watu wa kabila la Dani kwenye milima. Hawakuwaruhusu kuja kuishi katika inchi ya bonde. Waamori waliendelea kuishi katika miji iliyokuwa katika kilima cha Heresi, Ayaloni na Salabimu. Lakini watu wa makabila ya Manase na Efuraimu waliwatawala Waamori na kuwatumikisha kazi za kulazimishwa. Mupaka wa Waamori ulikuwa upande wa kaskazini ya Sela, kupitia njia inayopanda kwenda Akarabimu. Malaika wa Yawe aliondoka Gilgali, akaenda Bokimu, akawaambia Waisraeli: “Niliwaondoa katika inchi ya Misri na kuwaleta katika inchi ambayo niliahidi kwa kiapo kwa babu zenu. Nilisema kwamba sitalivunja agano langu nanyi hata kidogo. Na kwa upande wenu niliwaamuru musifanye agano na wenyeji wa inchi hii na kwamba mazabahu zao mutazibomoa. Lakini ninyi hamukuitii amri yangu. Kwa nini mambo haya? Kwa hiyo sasa ninasema: Sitawafukuza tena wakaaji wa inchi hii lakini watawataabisha ninyi, na miungu yao itakuwa mutego kwenu.” Malaika wa Yawe alipowaambia watu wote wa Israeli maneno haya, wakalalamika na kulia. Wakapaita pahali pale Bokimu, ni kusema “Wanaolia”. Pale wakamutolea Yawe sadaka. Yoshua aliwatuma Waisraeli wote waende kwenye maeneo yao waliyogawanyiwa kwa kurizi inchi. Waisraeli walimutumikia Yawe siku zote za maisha ya Yoshua na nyuma ya kifo chake kwa muda wote wale wazee waliobaki waliishi ambao waliyaona matendo makubwa ambayo Yawe aliwatendea Waisraeli. Yoshua mwana wa Nuni, na mutumishi wa Yawe, akakufa akiwa na umri wa miaka mia moja na kumi. Wakamuzika katika sehemu aliyogawanyiwa ikuwe yake kule Timunati-Heresi, katika inchi ya milima ya Efuraimu upande wa kaskazini wa mulima Gasi. Kisha watu wote wa kizazi chake wakakufa, kizazi kingine kikafuata ambacho hakikumujua Yawe wala matendo aliyowatendea watu wa Israeli. Basi, Waisraeli walitenda uovu mbele ya Yawe na kuabudu Mabali. Walimwacha Yawe, Mungu wa wazee wao, ambaye aliwaondoa katika inchi ya Misri, wakaifuata miungu mingine, miungu iliyoabudiwa na watu walioishi kandokando yao. Waliinama mbele ya miungu hiyo, wakamukasirikisha sana Yawe. Walimwacha Yawe, wakatumikia Mabali na Mastaroti. Basi, hasira ya Yawe ikawaka juu ya Israeli, naye akawaacha wanyanganyi wanyanganye mali zao. Akawatoa kwa waadui zao waliowazunguka hata wasiweze tena kuwashinda. Kila mara walipokwenda kupigana, mukono wa Yawe ulipambana nao kwa kuwaletea hasara, kama alivyokuwa amewaonya na kuapa. Nao wakakuwa katika huzuni kubwa. Halafu Yawe akawapa waamuzi ambao waliwaokoa toka katika mikono ya watu walionyanganya mali zao. Hata hivyo, Waisraeli hawakuwasikiliza waamuzi wao, maana walifanya kama wazinzi kwa kufuata miungu mingine na kuinama mbele yao. Wakaacha upesi njia ya babu zao. Babu zao walitii amri za Yawe lakini wao hawakuzitii. Kila mara Yawe alipowapelekea mwamuzi, yeye mwenyewe alikuwa pamoja na mwamuzi yule, akawaokoa toka katika mikono ya waadui zao muda wote wa maisha ya mwamuzi yule. Ingawa hivyo, Yawe aliwaonea huruma aliposikia kilio chao kutokana na mateso na masumbuko yao. Lakini kila mara mwamuzi alipokufa walirudilia mienendo yao ya zamani, wakaishi vibaya kuliko babu zao. Waliifuata miungu mingine, wakaitumikia na kuinama mbele yao, wala hawakuyaacha matendo yao wala uasi wao. Kwa hiyo Yawe akawaka hasira juu ya Waisraeli, akasema: “Kwa sababu watu hawa wamevunja agano nililofanya na babu zao, wakakataa kutii sauti yangu, sitayafukuza tena mataifa ambayo Yoshua aliyaacha, wakati alipokufa. Nitayatumia mataifa hayo kuwajaribu Waisraeli nione kama watairudilia njia yangu kama babu zao au sivyo.” Basi, Yawe akayaacha mataifa hayo ambayo hakumupa Yoshua ushindi juu yao, wala hakuyafukuza mara moja. Yawe aliyaacha kwa kuwajaribu Waisraeli ambao walikuwa hawajapigana vita katika inchi ya Kanana. Alifanya hivyo kusudi awape watu wa vizazi hivyo ujuzi wa kupigana maana hawakukuwa wameona vita. Aliacha mataifa ya watu hawa: wakubwa watano wa Wafilistini, Wakanana wote, Wasidoni na Wahivi waliohamia katika milima ya Lebanoni kutoka mulima Bali-Hermoni mpaka kufikia Hamati. Yawe alikusudia kuwatumia hao kusudi awajaribu Waisraeli, aone kama watatii amri zake alizowaamuru wazee wao kwa njia ya Musa. Basi, Waisraeli waliishi pamoja na Wakanana, Wahiti, Waamori, Waperizi, Wahivi na Wayebusi. Wakaoa wabinti zao na kuoesha wabinti zao kwa vijana wa mataifa hayo na kuiabudu miungu yao. Waisraeli walitenda uovu mbele ya Yawe. Wakamusahau Yawe, Mungu wao, wakaabudu Mabali na Maashera. Basi, hasira ya Yawe ikawaka juu ya Israeli, naye akawatia katika mikono ya mufalme wa Mesopotamia, jina lake Kusani, Yule-Mwovu-Sana. Wakamutumikia kwa muda wa miaka minane. Waisraeli wakamulilia Yawe, naye akawapelekea mutu wa kuwakomboa, ni kusema Otinieli mwana wa Kenazi, ndugu mudogo wa Kalebu. Basi, roho wa Yawe akamujaza Otinieli, naye akakuwa mwamuzi wa Waisraeli. Otinieli alikwenda katika vita naye Yawe akamutia Kusani, Yule-Mwovu-Sana, ufalme wa Mesopotamia, katika mikono yake. Inchi ikakuwa na amani kwa muda wa miaka makumi ine. Kisha Otinieli mwana wa Kenazi, akakufa. Waisraeli walitenda tena uovu mbele ya Yawe. Yawe akamutia nguvu mufalme wa Moabu aliyeitwa Mwana-Ngombe kusudi awashambulie Waisraeli, kwa sababu walitenda uovu mbele ya Yawe. Mufalme Mwana-Ngombe akawakusanya Waamori na Waamaleki, akaenda kupigana na Waisraeli, akawashinda. Akauteka Muji wa Miti ya Ngazi, ni kusema Yeriko. Waisraeli wakamutumikia Mwana-Ngombe, mufalme wa Moabu, kwa muda wa miaka kumi na minane. Lakini Waisraeli walipomulilia Yawe, basi, aliwapelekea mutu wa kuwakomboa, ni kusema Ehudu, mwana wa Gera wa kabila la Benjamina. Alikuwa mwenye kutumikisha zaidi mukono wa kushoto. Waisraeli wakamutuma apeleke zawadi zao kwa Mwana-Ngombe, mufalme wa Moabu. Ehudu akajitengenezea upanga wenye makali ngambo mbili; urefu wake sentimetre makumi tano. Akaufunga kwenye kiuno chake upande wa kuume ndani ya nguo yake. Kisha akamupelekea Mwana-Ngombe zile zawadi. Mwana-Ngombe alikuwa mutu munene sana. Ehudu alipomaliza kutoa zawadi, akawaambia watu waliobeba zawadi waondoke. Lakini yeye alipofika kwenye sanamu za mawe yaliyochongwa karibu na Gilgali, akamurudilia Mwana-Ngombe akasema: “Nina ujumbe wa siri kwako, ee mufalme.” Mufalme akawaamuru watumishi wakae kimya, nao wakatoka inje. Naye Ehudu akamukaribia pale alipokaa katika chumba chake chenye baridi katika baraza, akamwambia: “Nina ujumbe wako kutoka kwa Mungu.” Mufalme akasimama toka juu ya kiti chake. Ehudu akauchomoa upanga wake kwa mukono wake wa kushoto kutoka paja lake la kuume, akamuchoma nao katika tumbo lake. Upanga ukaingia ndani pamoja na mupini wake, mafuta yakaufunika upanga ule maana Ehudu hakuutoa tena; ukakuwa umetokea kwa nyuma. Kisha, Ehudu akatoka inje ndani ya baraza kisha kuifunga milango ya chumba hicho kwa ufunguo. Ehudu alipoondoka, watumishi wa mufalme wakarudi. Walipoona milango yote ya chumba imefungwa, wakafikiri kwamba amekwenda kujisaidia kwenye choo mule ndani ya nyumba. Wakangojea mpaka wakaanza kuona wasiwasi. Walipoona hafungui, wakatwaa ufunguo na kufungua mulango. Wakamwona mufalme wao chini, naye amekufa. Walipokuwa wanangoja, Ehudu akatoroka akipitia kwenye sanamu za mawe, akaenda Seira. Alipofika kule akapiga baragumu katika inchi ya milima ya Efuraimu, nao Waisraeli wakateremuka pamoja naye kutoka kule kwenye milima naye akawatangulia. Akawaambia: “Munifuate, maana Yawe amewatia waadui zenu Wamoabu katika mikono yenu.” Wakamufuata mpaka kwenye kivuko cha Yordani na kukiteka toka katika mikono ya Wamoabu, wakazuia mutu yeyote kupita. Siku hiyo, wakawaua Wamoabu yapata elfu kumi, wote wenye afya na nguvu, wala hakuna hata mumoja aliyeponyoka. Siku hiyo Waisraeli wakawashinda Wamoabu. Inchi ikakuwa na amani kwa muda wa miaka makumi nane. Nyuma ya Ehudu mwana wa Anati, Samugari akakamata nafasi yake. Yeye aliwaua Wafilistini mia sita kwa fimbo ya kuchunga ngombe. Naye vilevile aliwakomboa Waisraeli. Nyuma ya kifo cha Ehudu, Waisraeli walitenda tena uovu mbele ya Yawe. Yawe akawatia katika mikono ya mufalme wa Kanana, jina lake Asikie, ambaye aliishi Hazori. Jemadari wa waaskari wake aliitwa Sisera, mukaaji wa Haroseti-Hagoimu. Mufalme Asikie alikuwa na magari ya vita mia tisa ya chuma. Aliwagandamiza sana Waisraeli kwa miaka makumi mbili; nao wakamulilia Yawe awasaidie. Wakati ule, kulikuwa nabii mumoja mwanamuke aliyeitwa Debora, muke wa Lapidoti, aliyekuwa mwamuzi wa Waisraeli wakati ule. Debora alikuwa anazoea kuikaa chini ya muti wa ngazi uliokuwa kati ya muji wa Rama na muji wa Beteli katika inchi ya milima ya Efuraimu. Watu wa Israeli walimufikia kusudi awaamulie mashauri yao. Siku moja akamwita Baraka mwana wa Abinoamu wa Kedesi katika inchi ya Nafutali. Alipokuja akamwambia: “Yawe, Mungu wa Israeli, anakuamuru hivi: ‘Kwenda ukusanye watu wako kwenye mulima Tabori, uchague watu elfu kumi kutoka makabila ya Nafutali na Zebuluni. Mimi nitamuchochea Sisera, jemadari wa waaskari wa mufalme Asikie, akuje na waaskari na magari yake kupigana nawe kwenye muto Kisoni, na kumutia katika mikono yako.’ ” Baraka akamwambia Debora: “Kama utakwenda pamoja nami, nitakwenda. Lakini usipokwenda pamoja nami, sitakwenda.” Debora akamujibu: “Sawa. Nitakwenda pamoja nawe; lakini hautapata heshima yoyote ya ushindi, maana Yawe, atamutia Sisera katika mikono ya mwanamuke.” Basi, Debora akafuatana na Baraka kwenda Kedesi. Baraka akayaita makabila ya Nafutali na Zebuluni kule Kedesi. Watu elfu kumi wakamufuata. Debora akaenda pamoja naye. Wakati ule, Mukeni mumoja aliyeitwa Heberi alikuwa amejitenga na Wakeni wenzake ambao ni wazao wa Hobabu, baba mukwe wa Musa. Alikuwa amepiga hema lake mbali kule kwenye muti wa mwalo wa Sananimu, karibu na Kedesi. Sisera alipopata habari kwamba Baraka mwana wa Abinoamu amekwenda kwenye mulima Tabori, akakusanya waaskari wake wote na magari yake mia tisa ya chuma, akaondoka Haroseti-Hagoimu, akaenda kwenye muto Kisoni. Debora akamwambia Baraka: “Simama! Leo ni siku ambayo Yawe atamutia Sisera katika mikono yako. Yawe anakwenda mbele yako.” Basi, Baraka akashuka kutoka kwenye mulima Tabori akiwaongoza watu wake elfu kumi. Baraka akafanya mashambulizi, naye Yawe akamukimbiza Sisera na waaskari wake wote mbele ya Baraka kwa upanga. Sisera akatoka katika gari lake, akakimbia kwa miguu. Baraka akawafuatilia waaskari wale na magari mpaka Haroseti-Hagoimu na kuwaua waaskari wote wa Sisera kwa mapanga. Hakukubaki hata mutu mumoja. Lakini Sisera akakimbia kwa miguu mpaka katika hema ya Yaeli, muke wa Heberi Mukeni. Alifanya hivyo kwa sababu kulikuwa amani kati ya mufalme Asikie wa Hazori na jamaa ya Heberi. Yaeli akaenda kumupokea Sisera, akamwambia: “Bwana wangu, karibu kwangu, wala usiogope.” Akaingia ndani ya hema yake. Yaeli akamufunika kwa blanketi. Sisera akamwambia Yaeli: “Tafazali, unipe maji kidogo nikunywe, maana nina kiu.” Akamupa maziwa pahali pa maji, kisha akamufunika tena. Sisera akamwambia: “Simama kwenye mulango wa hema. Mutu yeyote akikuja kukuuliza kama kuna mutu yeyote hapa, umwambie hakuna.” Lakini Yaeli, muke wa Heberi, akatwaa musumari wa kufungia hema na nyundo, akamwendea polepole akaupigilia ule musumari wa kufungia hema katika paji la uso wake ukapenya mpaka katika udongo, kwa maana alikuwa amelala usingizi muzito sababu ya muchoko. Basi, Sisera akakufa palepale. Naye Baraka alipokuwa anamufuatilia Sisera, Yaeli akatoka inje kwa kumupokea akamwambia: “Ukuje nami nitakuonyesha yule unayemutafuta.” Baraka akaingia ndani ya hema la Yaeli na kumukuta Sisera chini, amekufa, na musumari wa hema ndani ya paji lake. Hivyo, siku hiyo Mungu akawapa Waisraeli ushindi juu ya mufalme Asikie wa Kanana. Waisraeli wakaendelea kumufuatilia Asikie, mufalme wa Kanana, mpaka walipomwangamiza. Siku hiyo, Debora na Baraka mwana wa Abinoamu, wakaimba wimbo huu: Viongozi walijitokeza kuongoza Israeli, watu walijitolea kwa mapenzi yao. Mumushukuru Yawe! Musikilize, enyi wafalme! Mutege sikio, enyi wakubwa! Nitamwimbia Yawe, Mungu wa Israeli. Ee Yawe, ulipotoka kule Seiri, ulipoteremuka kwenye mulima Edomu, inchi ilitetemeka, mbingu zilidondosha maji, mawingu yakaiangusha mvua. Milima ilitikisika mbele yako Yawe, mulima Sinai mbele yako Yawe, Mungu wa Israeli. Katika siku za Samugari mwana wa Anati, katika wakati wa Yaeli, makundi ya watu yalikoma kupita katika inchi, wasafiri walipitia njia za pembenipembeni. Walimaji walitoweka, walitoweka katika Israeli, mpaka nilipotokea mimi Debora, mimi ninayekuwa mama wa Israeli. Walijichagulia miungu mipya, kukakuwa vita katika inchi. Lakini hakukupatikana mwenye upanga au ngao kati ya watu elfu makumi ine wa Israeli. Ninawapa heshima viongozi wa Israeli waliojitoa kwa mapenzi yao kati ya watu. Mushukuru Yawe! Enyi munaopanda juu ya punda weupe, enyi munaoikalia matandiko ya bei kali, enyi munaotembea katika njia, mutangaze jambo hilo! Kwenye visima vya maji, tangaza ushindi wa Yawe, ushindi kwa walimaji wake katika Israeli. Watu wa Yawe walishuka kwenye mulango wa muji. “Amuka, amuka, Debora! Amuka! Amuka uimbe wimbo! Amuka, Baraka mwana wa Abinoamu, uwakamate wafungwa wako. Mashujaa waliobaki waliteremuka. Watu wa Yawe walikwenda kumupigania na wenye nguvu. Kutoka Efuraimu waliteremuka katika bonde, wakafuata wandugu zao watu wa Benjamina; kutoka Makiri, majemadari walishuka, kutoka Zebuluni, wenye fimbo ya mutawala. Wakubwa wa Isakari wakafuata Debora, watu wa Isakari, waaminifu kwa Baraka, wakamufuata mbio mpaka katika bonde. Lakini kati ya ukoo za Rubeni kulikuwa kusitasita kwingi. Kwa nini walibaki katika mazizi? Kwa kusikiliza milio ya kondoo? Kati ya ukoo za Rubeni kulikuwa kusitasita kwingi. Kabila la Gileadi lilibaki ngambo ya Yordani. Kabila la Dani, kwa nini mulibaki ndani ya mashua? Kabila la Aseri lilitulia kule pembeni ya bahari, lilikaa katika kivuko chake. Watu wa Zebuluni ni watu waliohatarisha maisha yao katika kifo. Hata wa Nafutali walisogelea kifo kwenye miinuko ya mashamba. “Kule Tanaki, pembeni ya chemichemi za Megido, wafalme walikuja, wakapigana; wafalme wa Kanana walipigana, lakini hawakuteka feza. Nyota kutoka mbinguni zilishiriki vita, zilifuata njia zao zikapigana na Sisera. Mafuriko ya muto Kisoni yaliwapeleka mbali, mafuriko makali ya muto Kisoni. Songa mbele kwa nguvu, ee nafsi yangu! “Farasi walipita wakipiga udongo, walipigapiga udongo na kishindo cha kwato zao. Malaika wa Yawe anasema hivi: ‘Ulaani muji wa Merosi, uwalaani vikali wakaaji wake; maana hawakukuja kumusaidia Yawe hawakumusaidia Yawe juu ya wenye nguvu’. “Abarikiwe kuliko wanawake wote Yaeli, muke wa Heberi Mukeni. Amebarikiwa kuliko wanawake wote wanaokaa katika mahema. Sisera alimwomba maji, naye akamupa maziwa; akamuletea siagi katika bakuli ya heshima. Kwa mukono mumoja akashika musumari wa kufungia hema, na kwa mukono wake wa kuume nyundo ya fundi. Alimuponda Sisera kichwa, akavunja na kupasuapasua paji lake. Sisera akainama, akaanguka; akalala kimya kwenye miguu yake. Hapo alipoinama ndipo alipoanguka amekufa! “Mama ya Sisera akaangalia toka kwenye dirisha, akachungulia, kisha akalalamika: ‘Kwa nini gari lake limechelewa? Mbona vishindo vya magari yake vimechelewa kusikilika?’ Jibu akalipata kwa wanawake wenye hekima: akajituliza tena na tena kwa jibu hilo: ‘Bila shaka wanatafuta na kugawanyana vitu: binti mumoja au wawili kwa kila askari, nguo ya sufu ya rangi kwa ajili ya Sisera, nguo ya sufu iliyopindwa vizuri, na mikufu miwili yenye kufumwa kwa ajili ya shingo yangu!’ “Ee Yawe, waangamie waadui zako wote! Lakini warafiki zako wakuwe kama jua, wakati linapochomoza kwa mwangaza mukubwa!” Inchi ya Waisraeli ikakuwa na amani kwa muda wa miaka makumi ine. Waisraeli walitenda uovu mbele ya Yawe; naye akawatia katika mikono ya Wamidiani kwa muda wa miaka saba. Wamidiani waliwagandamiza sana Waisraeli, mpaka wakajichimbia mashimo na mapango kwenye milima kuwa makimbilio yao. Kila mara Waisraeli walipopanda mbegu katika mashamba, Wamidiani, Waamaleki na watu wengine wa kule upande wa mashariki walikuja kuwashambulia. Mataifa hayo yaliweka kambi katika inchi, yakawashambulia na kuharibu mazao yote ya inchi hata kwenye mupaka wa Gaza, hawakuwaachia Waisraeli chochote, ikuwe kondoo, ngombe au punda. Waadui waliozoea kuja kwa wingi kama nzige, pamoja na ngombe na ngamia wao na kufanya makao yao katika inchi ya Israeli, waliharibu inchi ya Israeli kwa vile walikuwa wengi sana wasiohesabika. Waisraeli wakafanywa kuwa wamasikini sana na Wamidiani hata wakamulilia Yawe awasaidie. Waisraeli walipomulilia Yawe awaondolee taabu walizopata kwa Wamidiani, Yawe akawapelekea nabii, naye akawaambia: “Yawe, Mungu wa Israeli, anasema hivi: ‘Niliwaondoa katika inchi ya Misri ambako mulikuwa watumwa, nikawakomboa toka katika mikono ya Wamisri wote waliowagandamiza. Nikawafukuza watu mbele yenu na kuwapa ninyi inchi yao. Kisha nikawakumbusha kwamba mimi ni Yawe, Mungu wenu, na kwamba musiiheshimu miungu ya Waamori, ambao inchi yao mumeitwaa, lakini hamukuisikiliza sauti yangu.’ ” Malaika wa Yawe akaenda, akaikaa chini ya muti wa mwalo wa Yoasi Mwabiezeri, kule Ofura. Gideoni mwana wa Yoasi alikuwa anapepeta ngano ndani ya kikamulio cha kukamulia zabibu kusudi Wamidiani wasimwone. Malaika wa Yawe akamutokea, akamwambia: “Yawe yuko pamoja nawe, ewe shujaa.” Gideoni akamwambia: “Ee Bwana wangu, ikiwa Yawe yuko pamoja nasi, mbona mambo haya yote yametupata? Yako wapi matendo yake ya ajabu ambayo wazee wetu walituelezea, wakisema: ‘Yawe ndiye aliyetutoa katika inchi ya Misri.’ Lakini sasa Yawe ametutupilia na kututia katika mikono ya Wamidiani!” Yawe akamugeukia, akamwambia: “Kwenda kwa uwezo unaokuwa nao, uikomboe Israeli kutoka Wamidiani. Ni mimi ninayekutuma.” Gideoni akamujibu: “Tafazali Bwana, nitaweza namna gani kuikomboa Israeli? Ukoo wangu ndio wa bure zaidi katika kabila la Manase, na mimi mwenyewe ni mudogo kabisa katika jamaa yetu!” Yawe akamwambia: “Nitakuwa pamoja nawe; nawe utawaangamiza Wamidiani sawa vile wangekuwa mutu mumoja.” Gideoni akamwambia: “Basi, ikiwa nimepata rehema kwako, unionyeshe kitambulisho kusudi nijue kwamba ni wewe kweli uliyezungumuza nami. Ninakuomba usiondoke hapa mpaka nitakaporudi na kukuletea zawadi yangu na kuiweka mbele yako.” Naye akamujibu: “Nitakaa hapa mpaka utakaporudi.” Gideoni akaenda kwake, akatayarisha mwana-mbuzi na mikate isiyotiwa chachu kutoka debe la unga. Akatia nyama ndani ya kikapu na muchuzi ndani ya chungu, kisha akamupelekea chini ya muti wa mwalo, akamupa. Malaika wa Mungu akamwambia: “Twaa nyama na mikate isiyotiwa chachu uviweke juu ya jiwe hili. Halafu tia muchuzi juu ya mikate na nyama.” Naye akafanya hivyo. Malaika wa Yawe akanyoosha fimbo yake, akagusa nyama na mikate kwa incha ya fimbo. Kwa rafla, moto ukatoka ndani ya jiwe, ukateketeza nyama na mikate. Mara moja malaika wa Yawe akatoweka mbele yake. Halafu Gideoni akatambua kwamba huyo alikuwa malaika wa Yawe; akasema: “Ole wangu, ee Bwana wangu Yawe, maana nimemwona malaika wako uso kwa uso.” Lakini Yawe akamwambia: “Amani ikuwe nawe! Usiogope, hautakufa.” Gideoni akamujengea Yawe mazabahu kule na kuyaita, “Yawe ni Amani.” Mazabahu hiyo iko kule Ofura, muji wa Waabiezeri, mpaka leo. Usiku ule, Yawe akamwambia Gideoni: “Twaa ngombe dume mumoja wa baba yako, ngombe dume yule wa pili wa umri wa miaka saba. Bomoa mazabahu ya mungu Bali baba yako anayokuwa nayo na kuvunja sanamu ya mungu Ashera inayokuwa karibu nayo. Halafu, unijengee mimi Yawe, Mungu wako, mazabahu nzuri juu ya mwinuko ule. Kisha unitolee sadaka ya kuteketezwa ya yule ngombe dume wa pili ukitumia kuni za ile sanamu ya Ashera uliyoivunja.” Basi, Gideoni akatwaa watumishi wake kumi, akafanya kama vile alivyoagizwa na Yawe. Lakini kwa sababu aliiogopa jamaa yake na watu wa muji, pahali pa kufanya hayo muchana, akayafanya wakati wa usiku. Wakaaji wa muji walipoamuka asubui mapema waliona mazabahu ya Bali na sanamu ya Ashera iliyokuwa karibu nayo vimeharibiwa. Yule ngombe dume wa pili alikuwa ameteketezwa juu ya mazabahu iliyokuwa imejengwa pahali pale. Wakaulizana: “Ni nani amefanya jambo hili?” Walipofanya uchunguzi wakagundua kwamba ni Gideoni mwana wa Yoasi ndiye aliyekuwa amefanya hayo. Wakaaji wa muji wakamwendea Yoasi, wakamwambia: “Umutoe mwana wako tumwue, maana ameharibu mazabahu ya mungu Bali na kuivunja sanamu ya mungu Ashera iliyokuwa karibu nayo.” Yoasi akawaambia wale wote waliomufuata: “Muko munamutetea Bali? Ninyi, mutamwokoa? Yeyote atakayemutetea atauawa mbele ya mapambazuko. Kama Bali ni mungu, basi, ajitetee mwenyewe maana mazabahu yake imebomolewa.” Siku hiyo wakamwita Gideoni “Yerubali” maana yake “Bali ajitetee”, maana aliibomoa mazabahu ya mungu Bali. Wamidiani, Waamaleki na watu wote wanaokaa pembeni ya muto Yordani wakapiga kambi zao katika bonde la Yezereheli. Lakini roho wa Yawe akamujaza Gideoni. Gideoni akapiga baragumu kwa kuwaita Waabiezeri wakuje kumufuata. Akatuma wajumbe katika inchi yote ya Manase wakuje kumufuata. Wajumbe wengine akawatuma kuwaita watu wa makabila ya Aseri, Zebuluni na Nafutali, nao wakakuja kujiunga naye. Gideoni akamwambia Mungu: “Ikiwa utaikomboa Israeli kwa mukono wangu kama ulivyosema, sasa ninaweka ngozi ya kondoo chini kwenye kiwanja cha kupepetea ngano. Ikiwa kutakuwa umande juu ya ngozi tu, na udongo unaouzunguka ikakuwa mukavu, basi, nitajua kwamba utawaokoa Waisraeli kwa mukono wangu kama ulivyosema.” Ikakuwa hivyo, kwa maana alipoamuka asubui kesho yake, alikamua umande uliokuwa juu ya ile ngozi, akajaza bakuli. Gideoni akamwambia Mungu: “Tafazali, usinikasirikie. Ninakuomba niseme mara moja tena. Ninakuomba uniruhusu nitumie ngozi hii kwa kufanya jaribio lingine. Ninakuomba juu ya ngozi kukuwe kukavu, lakini kwenye udongo kukuwe umande.” Mungu akafanya hivyo usiku ule, maana juu ya ngozi kulikuwa kukavu na kwenye udongo kulikuwa umande. Yerubali, ni kusema Gideoni na watu wote waliokuwa pamoja naye wakaamuka mapema, wakapiga kambi yao katika bonde karibu na chemichemi ya Harodi. Kambi ya Wamidiani ilikuwa upande wao wa kaskazini katika bonde karibu na mulima More. Yawe akamwambia Gideoni: “Watu unaokuwa nao ni wengi sana kwangu mimi kwa kuwatia Wamidiani katika mikono yao. Waisraeli wasipate kujisifu mbele yangu na kusema kwamba wamejiokoa kwa nguvu zao wenyewe. Sasa uwatangazie watu wote kwamba mutu yeyote anayekuwa mwoga au anayetetemeka arudi kwake.” Basi, Gideoni akawajaribu, na watu elfu makumi mbili na mbili wakarudi kwao, akabaki na watu elfu kumi. Yawe akamwambia Gideoni: “Watu hao wangali wengi sana. Sasa uwapeleke kwenye muto, nami nitawajaribu kule. Mutu yeyote nitakayekuambia: ‘Huyu atakwenda nawe, huyo aende nawe. Lakini mutu yeyote nitakayekuambia hatakwenda nawe, huyo asiende nawe.’ ” Basi, Gideoni akawapeleka watu kwenye muto na Yawe akamwambia: “Watu watakaolamba maji kwa ulimi kama imbwa, utawatenganisha na wale watakaopiga magoti kwa kunywa maji.” Jumla ya waliokunywa maji kwa kuchota kwa mikono yao na kulamba kama imbwa ilikuwa mia tatu. Lakini wengine wote waliobaki walipiga magoti kwa kunywa maji. Yawe akamwambia Gideoni: “Kwa hao watu mia tatu waliokunywa kwa kulamba kama imbwa, nitawaokoa Waisraeli na kuwatia Wamidiani katika mikono yao. Lakini wale wengine wote warudie kwao.” Basi, Gideoni akatwaa vyakula vya wale waliokuwa wanaondoka na baragumu, akawaaga waende kwao. Yeye akabaki na wale watu mia tatu. Kambi ya Wamidiani ilikuwa katika bonde upande wao wa chini. Usiku ule, Yawe akamwambia Gideoni: “Kwenda uwashambulie katika kambi yao, maana nimewatia katika mikono yako. Lakini kama unaogopa, kwenda pamoja na mutumishi wako Pura. Kule utasikia wanayosema, nawe utapata nguvu za kuweza kwenda kuwashambulia.” Basi, Gideoni akaenda pamoja na mutumishi wake Pura mpaka kwenye vituo vya walinda zamu wa kambi ya Wamidiani. Wamidiani, Waamaleki na watu wote wa mashariki walilala katika bonde, wengi kama nzige, na ngamia wao wasiohesabika, wengi kama muchanga wa bahari. Gideoni alipofika, akamusikia mutu mumoja akisimulia na mwenzake juu ya ndoto yake hivi: “Niliota ndoto. Nikaona mukate wa shayiri ukiviringikaviringika mpaka katika kambi ya Wamidiani, ukalipiga hema na kulipindua machali juu. Hema likalala chini.” Mwenzake akamujibu; “Hiyo inamaanisha tu upanga wa yule Mwisraeli Gideoni mwana wa Yoasi ambaye Mungu amewatia Wamidiani pamoja na waaskari wote katika mikono yake.” Gideoni aliposikia masimulizi hayo ya ndoto na mafasirio yake, akamwabudu Mungu. Kisha akarudi kwenye kambi ya Waisraeli, akasema: “Musimame tuende, maana Yawe amelitia jeshi la Wamidiani katika mikono yenu.” Basi akawagawanya wale watu mia tatu katika makundi matatu, akawapa baragumu na mitungi yenye mienge. Akawaambia: “Muniangalie na kufanya sawa vile nitakavyofanya wakati nitakapofika katika kambi. Nitakapopiga baragumu, mimi pamoja na kundi langu, ninyi wote mupige baragumu kutoka kila upande na kusema kwa sauti kubwa: ‘Kwa ajili ya Yawe na kwa ajili ya Gideoni!’ ” Ilipokaribia saa sita za usiku, Gideoni na kundi lake la watu mia moja wakafika kwa mwisho wa kambi, kwa mwanzo wa zamu ya kati. Wakati walipokuwa wamebadilisha wenye zamu, wakakaribia kambi ya waadui. Wakapiga baragumu na kuvunja mitungi waliyokuwa nayo. Makundi yote matatu kwa pamoja yakapiga baragumu na kuvunja mitungi yao. Katika mikono yao ya kushoto walishika mienge na kwa mikono yao ya kuume baragumu na kuzipiga, na walikuwa wanasema kwa sauti kubwa: “Upanga kwa ajili ya Yawe na kwa ajili ya Gideoni!” Wakasimama kila mumoja kwa nafasi yake kuizunguka kambi. Jeshi lote la waadui likatawanyika nalo likilalamika. Watu wa Gideoni walipopiga baragumu zao mia tatu, Yawe akawafanya Wamidiani waanze kuuana wao kwa wao katika kambi. Waliobaki wakatoroka mpaka Zerera, wakafika Beti-Sita, hata kwenye mupaka wa Abeli-Mehola karibu na Tabati. Waisraeli wa kabila la Nafutali, Aseri, na Manase, wote waliitwa, wakawafuatilia Wamidiani. Gideoni akatuma wajumbe katika inchi yote ya milima ya Efuraimu watangaze: “Muteremuke kwa kuwafuata Wamidiani na kuwazuia kwa kuteka vijito na muto Yordani mpaka Beti-Bara.” Basi, wanaume wote wa Efuraimu wakakuja na kuuteka muto Yordani mpaka Beti-Bara. Wakatwaa mateka viongozi wawili wa Midiani, majina yao ni Kibombobombo na Imbwa-wa-Pori. Wakamwua Kibombobombo juu ya jiwe la Kibombobombo, naye Imbwa-wa-Pori wakamwua katika kikamulio cha Imbwa-wa-Pori wakiwa wanawafuatilia Wamidiani. Wakamuletea Gideoni vichwa vya Kibombobombo na Imbwa-wa-Pori, ngambo ya muto Yordani. Watu wa kabila la Efuraimu wakamwuliza Gideoni: “Kwa nini umetutendea hivyo? Kwa nini haukutuita ulipokwenda kupigana na Wamidiani?” Wakamugombeza kwa ukali. Lakini Gideoni akawajibu: “Mambo niliyofanya mimi si kitu kabisa yakilinganishwa na yale muliyoyafanya ninyi. Walichookota watu wa Efuraimu wakati wa mavuno ni kizuri kuliko mavuno ya jamaa yangu ya Abiezeri. Mungu amewatia katika mikono yenu wale wakubwa wa Midiani, Kibombobombo na Imbwa-wa-Pori. Basi, mimi nimefanya nini nikilinganishwa nanyi?” Gideoni alipokwisha kusema hivyo, hasira yao juu yake ikatulia. Gideoni na wenzake mia tatu wakafika Yordani, wakavuka. Ingawa walikuwa wamechoka sana, waliendelea kuwafuatilia waadui zao. Basi, akawaambia watu wa Sukoti: “Tafazali, muwape wenzangu hawa mikate maana wamechoka sana; nami ninaendelea kuwafuatilia Sadaka na Kivuli, wafalme wa Midiani?” Lakini viongozi wa Sukoti wakamwuliza: “Kwa nini tuwape mikate nanyi hamujamushinda Sadaka na Kivuli?” Gideoni akawaambia: “Sawa, lakini Yawe atakapowatia Sadaka na Kivuli katika mikono yangu, nitaichanachana miili yenu kwa miiba na michongoma za jangwa.” Kutoka kule akawaendea watu wa Penueli, akawaomba namna ileile. Nao watu wa Penueli wakamujibu kama vile watu wa Sukoti walivyomujibu. Gideoni akawaambia: “Nitakaporudi kwa amani nitaubomoa munara huu.” Sadaka na Kivuli walikuwa kule Karkori pamoja na jeshi lao la watu elfu kumi na tano ambao ndio tu waliobaki kutoka jeshi la upande wa mashariki, maana wenzao elfu mia moja na makumi mbili waliuawa. Gideoni akafuata njia ya upande wa magaribi inayokuwa upande wa mashariki wa Noba na Yogibeha, akalishambulia jeshi hilo ambalo halikukuwa tayari. Sadaka na Kivuli, wafalme wa Midiani, walitoroka wakakimbia, lakini Gideoni akawafuatilia, akawakamata na kulitia jeshi lote hofu kubwa. Kisha, Gideoni mwana wa Yoasi, akarudi kutoka katika vita akipitia kwenye muteremuko wa Heresi. Akamukamata kijana mumoja wa Sukoti na kumwulizauliza. Kijana huyo akamwandikia majina ya viongozi na wazee wakubwa wa Sukoti, jumla yao watu makumi saba na saba. Gideoni akarudi kwa watu wa Sukoti, akawaambia: “Si mutakumbuka mulivyonitukana muliposema: ‘Kwa nini tuwape mikate watu wako waliochoka sana nanyi hamujamushinda Sadaka na Kivuli?’ Haya basi, Sadaka na Kivuli ndio hawa.” Basi, akawatwaa wazee wa Sukoti na kuwapa fundisho wanaume wote kwa kuichana miili yao kwa miiba na michongoma. Vilevile akaubomoa munara wa Penueli na kuwaua wakaaji wa muji ule. Kisha, akawauliza Sadaka na Kivuli: “Watu wale muliowaua kule Tabori walikuwa namna gani?” Wakamujibu: “Walifanana na wewe, maana walionekana kama wana wa mufalme.” Naye akawaambia: “Hao walikuwa wandugu zangu, wana wa mama yangu muzazi. Kama vile Yawe anavyoishi, kama musingewaua, hata mimi nisingewaua ninyi.” Kisha akamwambia Yeteri, muzaliwa wake wa kwanza: “Simama, uwaue.” Lakini Yeteri akaogopa kutwaa upanga wake maana alikuwa angali kijana. Hapo Sadaka na Kivuli wakasema: “Utuue wewe mwenyewe, maana hii ni kazi ya mutu muzima.” Gideoni akawaua yeye mwenyewe na kutwaa mapambo yao yaliyokuwa kwenye shingo la ngamia wao. Kisha, Waisraeli wakamwambia Gideoni: “Wewe ukuwe mutawala wetu, na nyuma yako wazao wako watutawale, kwa sababu wewe umetukomboa kutoka kwa Wamidiani.” Gideoni akawajibu: “Mimi sitakuwa mutawala wenu wala mwana wangu hatakuwa mutawala wenu. Yawe ndiye atakayekuwa mutawala wenu.” Kisha akawaambia: “Ningependa kuwaomba kitu kimoja; ninaomba kila mumoja wenu anipe pete kati ya vitu mulivyoteka.” Wale Wamidiani kwa vile walikuwa Waisimaeli, walivaa pete za zahabu. Watu wakamujibu: “Tutakupa pasipo kunungunika.” Wakatandaza nguo na kila mumoja akatupa pale pete walizokuwa wameteka. Uzito wa pete zote alizoomba wamupe ulikuwa kilo makumi mbili. Zaidi ya hivyo, alipokea vilevile vyuma vya masikio, nguo za rangi nyekundu-nyeusi zilizovaliwa na wafalme wa Midiani na mikufu iliyokuwa kwenye shingo za ngamia wao. Gideoni akazitumia kwa kutengenezea kizibao ambacho alikiweka kwenye muji wake wa Ofura. Waisraeli wote wakaenda kule kukiabudu. Kizibao hicho kikakuwa mutego kwa Gideoni na jamaa yake. Basi, Wamidiani walishindwa kabisa nao hawakuweza kujiinua juu hata kidogo. Inchi ya Israeli ikakuwa na amani kwa muda wa miaka makumi ine. Gideoni, ni kusema Yerubali mwana wa Yoasi, akarudi kwake na kukaa kule. Gideoni alikuwa na watoto wanaume makumi saba, maana alioa wanawake wengi. Alikuwa na habara kule Sekemu ambaye alimuzalia mutoto mwanaume, jina lake Abimeleki. Gideoni mwana wa Yoasi, akakufa akiwa na umri mukubwa, akazikwa katika kaburi la baba yake Yoasi kwenye muji wa Ofura wa Waabiezeri. Nyuma ya kifo cha Gideoni, Waisraeli wakairudilia miungu ya Bali na kuiabudu. Wakamufanya Bali-Beriti kuwa mungu wao. Waisraeli wakamusahau Yawe, Mungu wao, aliyewakomboa kutoka kwa waadui zao wengi waliowazunguka kila upande. Tena, hawakuitendea mema jamaa ya Yerubali, ni kusema Gideoni kwa mema yote aliyoyatenda katika Israeli. Abimeleki mwana wa Gideoni, akawaendea wandugu na wana wote wa kabila za mama yake kule Sekemu, akawaambia: “Museme hapa hapa mbele ya wanainchi wote wa Sekemu: Jambo gani ni jema kwenu, kwamba watoto wote makumi saba wa kiume wa Yerubali wawatawale au mutoto mumoja? Mukumbuke kwamba mimi ni damu yenu.” Wandugu za mama yake wakatangaza maneno popote kule Sekemu kwa jina lake, na watu wote wa Sekemu wakaamua kumufuata maana alikuwa ndugu yao. Wakamupa vikoroti makumi saba vya feza vilivyokuwa kwenye nyumba ya Bali-Beriti ambavyo alivitumia kwa kulipa watu wakorofi na watu ovyoovyo kusudi wamufuate. Akafuatana nao kwenda Ofura kwa baba yake naye akawaua wandugu zake wote makumi saba juu ya jiwe moja. Lakini Yotamu, mwana mudogo wa Yerubali aliponyoka kufa, maana alijificha. Wanainchi wote wa Sekemu na Beti-Milo wakakusanyika kwenye muti wa mwalo unaokuwa karibu na munara kule Sekemu, wakamufanya Abimeleki kuwa mufalme wao. Yotamu alipopata habari hiyo, alikwenda kusimama juu ya mulima Gerizimu, akasema kwa sauti kubwa: “Munisikilize, enyi watu wa Sekemu kama munataka Mungu awasikilize. Siku moja, miti ilikwenda kujitafutia mufalme. Basi, ikauambia muzeituni: ‘Utawale juu yetu!’ Lakini muzeituni ukajibu: ‘Munazani ninaweza kuacha shuguli yangu ya kuzalisha mafuta ambayo yanaheshimiwa sana na miungu na wanadamu niende kujisumbua kuitawala miti?’ Kisha miti ikauambia muti wa tini: ‘Ukuje wewe utawale juu yetu.’ Lakini muti wa tini ukajibu: ‘Munazani ninaweza kuacha shuguli yangu ya kuzalisha matunda mazuri na matamu, niende kujisumbua kuitawala miti?’ Halafu miti ikauambia muzabibu: ‘Ukuje wewe ukuwe mutawala juu yetu.’ Lakini muzabibu ukajibu: ‘Munazani ninaweza kuacha shuguli yangu ya kuzalisha divai ambayo inafurahisha miungu na wanadamu, niende kujisumbua kuitawala miti?’ Kwa mwisho miti yote ikauendea muti wa miiba na kuuambia: ‘Ukuje wewe utawale juu yetu.’ Muti wa miiba ukajibu: ‘Kama kweli munataka kunichagua kuwa mufalme, mukuje mukae chini ya kivuli changu. Lakini kama hamutaki kufanya hivyo, basi moto utoke kwenye miiba yangu na kuiteketeza hata mierezi ya Lebanoni.’ ” Yotamu akaendelea kusema: “Sasa basi, munazani mumefanya Abimeleki mufalme kwa nia njema na uaminifu? Munazani mumemutendea wema Yerubali na jamaa yake kama alivyostahili kwa matendo yake? Kwa maana baba yangu alihatarisha maisha yake kwa kuwapigania na kuwakomboa kutoka kwa Wamidiani! Lakini leo mumeishambulia jamaa ya baba yangu na kuwaua wana makumi saba juu ya jiwe moja, halafu mumemufanya Abimeleki mutoto wa mujakazi wa baba, akuwe mufalme wa wakaaji wa Sekemu kwa sababu tu ni mutu wa ukoo wenu. Sasa basi, kama mumetenda hayo kwa nia njema na kwa kumuheshimu Yerubali na jamaa yake, basi, mufurahi pamoja na Abimeleki, naye afurahi pamoja nanyi. Lakini, kama sivyo, moto utoke kwa Abimeleki na kuwateketeza wanainchi wa Sekemu na Beti-Milo, tena moto utoke kwa wanainchi wa Sekemu na Beti-Milo na kumuteketeza Abimeleki.” Kisha Yotamu akatoroka, akakimbilia Beri, akakaa kule, kwa maana alimwogopa ndugu yake Abimeleki. Abimeleki akatawala juu ya Israeli kwa muda wa miaka mitatu. Kisha Mungu akaleta roho ya uadui kati ya Abimeleki na watu wa Sekemu, nao wakamwasi. Ndivyo watu wa Sekemu pamoja na ndugu yao Abimeleki walivyoazibiwa kwa sababu waliwatendea kwa ukali wana makumi saba wa Yerubali. Azabu ya mauaji hayo iliwapata maana Abimeleki aliwaua akisaidiwa na hao watu wa Sekemu. Watu wa Sekemu waliweka washambulizi wamuvizie Abimeleki kutoka vilele vya mulima. Watu hao waliwanyanganya mali zao wote waliopita kule. Abimeleki alipata habari hii. Siku moja, Gali mwana wa Ebedi alikwenda pamoja na wandugu zake kukaa Sekemu. Watu wa Sekemu wakamuwekea tumaini. Wakatoka na kwenda kwenye mashamba yao ya mizabibu, wakachuma zabibu halafu wakazikamua, wakatengeneza divai wakafanya sikukuu. Wakaingia kwenye nyumba ya mungu wao wakakula na kunywa, kisha wakamutukana Abimeleki. Gali mwana wa Ebedi, akasema: “Abimeleki ni nani? Sisi hapa Sekemu ni watu wa aina gani hata tumutumikie Abimeleki? Gideoni na Zebuli jemadari wake walimutumikia Hamori baba wa Sekemu, lakini kwa nini basi, sisi tumutumikie Abimeleki? Kama watu hawa wangekuwa chini yangu, ningemwondoa Abimeleki. Ningemwambia Abimeleki: ‘Ongeza jeshi lako, kisha, ukuje mbele ya watu wote tupigane.’ ” Zebuli, mutawala wa muji, aliposikia maneno ya Gali mwana wa Ebedi, akakasirika sana. Basi akamupelekea Abimeleki ujumbe kule Aruma akasema: “Gali, mwana wa Ebedi, pamoja na wandugu zake wameingia katika muji wa Sekemu na kuchochea uasi juu yako. Basi, rudi wewe na watu unaokuwa nao, wakati wa usiku, uvizie katika mashamba karibu na muji. Mara jua litakapotoka wakati wa asubui, ushambulie muji. Gali akitoka pamoja na watu wake kuja kupigana nawe, uwatendee sawa unavyoweza.” Abimeleki akaondoka na watu waliokuwa pamoja naye kuja Sekemu wakati wa usiku. Aliwagawanya watu wake katika vikundi vine na kuvizia kule karibu na muji. Gali mwana wa Ebedi akatoka inje na kusimama kwenye mulango wa muji. Wakati ule Abimeleki na watu wake walitoka pahali walipokuwa wanavizia. Gali alipowaona, akamwambia Zebuli: “Angalia, watu wanashuka kutoka vilele vya mulima.” Zebuli akamwambia: “Wewe unaona vivuli vya milima sawa vile ni watu.” Gali akasema tena: “Angalia! Watu wanashuka katikati ya inchi na kikundi kingine kinatoka upande wa muti wa Mwalo wa Waaguzi.” Kisha Zebuli akamwambia: “Majivuno yako yako wapi sasa? Si ni wewe uliyesema: ‘Abimeleki ni nani? Kwa nini tumutumikie?’ Sasa, hao ndio watu uliowazarau. Kwenda upigane nao.” Gali akatoka akiwaongoza watu wa Sekemu na kupigana na Abimeleki. Kisha, Gali akakimbia mbele yake. Naye Abimeleki akamufuatilia. Watu wengi waliumizwa na kuanguka katika njia mpaka kwenye mulango wa muji. Abimeleki akakaa Aruma na Zebuli akamufukuza Gali na wandugu zake kutoka katika muji wa Sekemu. Siku iliyofuata, Abimeleki akapata habari kwamba watu wa Sekemu wametoka katika muji na kwenda katika mashamba. Akatwaa watu wake akawagawanya katika vikundi vine, kusudi waende kuvizia katika mashamba. Alipowaona watu wanatoka katika muji, akatoka alikojificha akawaua. Abimeleki na kundi lake wakaenda mbio kwenda kulinda mulango wa muji. Makundi yake mawili mengine yaliwashambulia wale waliokuwa katika mashamba na kuwaua. Abimeleki akapigana na wakaaji wa muji ule siku nzima. Akauteka muji na kuwaua watu wote waliokuwa humo. Akauteketeza muji kwa moto na kuutia chumvi. Watu wote waliokuwa katika munara wa Sekemu waliposikia habari hiyo, wakakimbilia kwenye chumba cha ndani cha nyumba ya mungu aliyeitwa Eli-Beriti. Abimeleki alipata habari kwamba watu wote waliokuwa kwenye munara wa Sekemu wamejikusanya pamoja. Abimeleki na watu wake wakaenda kwenye mulima Salmoni, akatwaa shoka, akakata tawi la muti na kuliweka juu ya bega lake. Halafu akawaambia wale watu aliokuwa nao waharakishe kufanya kama alivyofanya. Kila mumoja akakata tawi kama lile la Abimeleki. Wakabeba matawi yao na kuyaegemeza kwenye kuta za chumba kile, wakayatia moto na kuchoma chumba. Watu wote wanaume na wanawake yapata elfu moja waliokuwa katika munara wa Sekemu wakakufa. Kisha Abimeleki akaenda Tebesi, akazunguka muji ule na kuuteka. Lakini kulikuwa munara imara katikati ya muji. Basi, wakaaji wote wa muji huo wanaume na wanawake wakakimbilia humo na kujifungia ndani. Wakapanda kwenye paa la munara huo. Abimeleki akafika kwenye munara na kuushambulia. Kisha, akakaribia mulango wa munara autie moto. Mwanamuke mumoja akatupa jiwe la kusagia, akamuponda Abimeleki kichwa. Kisha Abimeleki akamwita haraka kijana wake aliyemubebea silaha akamwambia: “Twaa upanga wako uniue, watu wasipate kusema kwamba niliuawa na mwanamuke.” Kijana akatwaa upanga wake, akamuchoma na kumwua. Waisraeli walipoona kwamba Abimeleki amekufa, wakaondoka na kurudi kila mumoja kwake. Hivi ndivyo Mungu alivyomwazibu Abimeleki kwa kosa lake juu ya baba yake kwa kuwaua wandugu zake makumi saba. Vilevile Mungu akawafanya watu wa Sekemu waazibiwe kwa uovu wao walioufanya. Hivyo, laana ya Yotamu mwana wa Yerubali ikawapata. Nyuma ya kifo cha Abimeleki, Tola mwana wa Puha mujukuu wa Dodo, wa kabila la Isakari, akatokea kuwakomboa Waisraeli. Tola aliishi Samiri katika inchi ya milima ya Efuraimu. Alikuwa mwamuzi wa Israeli kwa miaka makumi mbili na mitatu, kisha akakufa na kuzikwa kule Samiri. Nyuma ya Tola, kukatokea Yairi wa Gileadi, akakuwa mwamuzi wa Waisraeli kwa miaka makumi mbili na mbili. Yairi alikuwa na watoto wa kiume makumi tatu ambao walipanda juu ya punda makumi tatu na walikuwa na miji makumi tatu katika inchi ya Gileadi, ambayo mpaka leo inaitwa Miji ya Yairi. Yairi akakufa na kuzikwa kule Kamoni. Waisraeli wakatenda tena uovu mbele ya Yawe, wakatumikia Mabali, Mastaroti, na miungu ya Aramu, ya Sidona, ya Moabu, ya Amoni na ya Wafilistini. Wakamwacha Yawe wala hawakumwabudu tena. Hasira ya Yawe ikawaka juu ya Waisraeli, naye akawatia katika mikono ya Wafilistini na Waamoni. Kwa miaka kumi na minane hao waliwatesa na kuwagandamiza Waisraeli walioishi kule Gileadi katika eneo la Waamori upande wa mashariki wa muto Yordani. Waamoni nao walivuka muto Yordani kupigana na makabila ya Yuda, Benjamina na Efuraimu. Nao Waisraeli wakapata taabu sana. Basi wakamulilia Yawe, wakisema: “Tumetenda zambi mbele yako, maana tumekuacha wewe Mungu wetu, tukatumikia Mabali.” Naye Yawe akawaambia: “Mimi sikuwakomboa kutoka kwa Wamisri, Waamoni, Waamori, na Wafilistini? Wasidoni, Waamaleki na Wamidiani waliwagandamiza nanyi mukanililia, nami nikawakomboa toka katika mikono yao. Hata hivyo ninyi mumeniacha, mukatumikia miungu mingine. Kwa hiyo sitawakomboa tena. Muende muililie hiyo miungu muliyoichagua. Muache hiyo iwakomboe katika taabu zenu!” Lakini Waisraeli wakamwambia Yawe: “Tumetenda zambi. Utufanye vile unavyopenda, lakini tunakuomba utuokoe leo.” Kisha wakaitupilia mbali miungu ya kigeni, wakamutumikia tena Yawe. Yawe hakuweza kuvumilia zaidi kuona taabu za Waisraeli. Waamoni wakajikusanya wakapiga kambi yao kule Gileadi. Waisraeli nao wakakusanyika na kupiga kambi yao kule Misipa. Waisraeli na viongozi wao wakaulizana: “Ni nani atakayeanza kupigana na Waamoni? Atakayefanya hivyo ndiye atakayekuwa kiongozi wa wakaaji wote wa Gileadi.” Kule Gileadi kulikuwa mupiganaji mumoja anayeitwa Yefuta, mwana wa mama mumoja kahaba, na baba yake aliitwa Gileadi. Gileadi alikuwa vilevile na wana wengine toka kwa muke wake. Watoto wa muke huyo walipokuwa wakubwa, wakamufukuza Yefuta kutoka kwao, wakamwambia: “Wewe hauna haki ya kupata urizi kutoka kwa baba yetu, maana wewe ni mutoto wa mwanamuke mwingine.” Basi, Yefuta akawakimbia wandugu zake akaenda kuishi katika inchi ya Tobu. Kule watu wa ovyo wakakusanyika kujiunga naye, wakamufuata katika safari zake za mashambulio. Nyuma ya muda fulani, Waamoni wakawashambulia Waisraeli. Wakati vita ilipopamba moto, wazee wa Gileadi wakaenda kumuleta Yefuta kutoka inchi ya Tobu, wakamwambia: “Kuja utuongoze katika vita yetu na Waamoni.” Lakini Yefuta akawaambia hao wazee wa Gileadi: “Si mulinichukia hata mukanifukuza kutoka kwa jamaa ya baba yangu? Kwa nini munanifikia sasa mukiwa katika taabu?” Hao wazee wa Gileadi wakamwambia: “Ndiyo maana tumekufikia kusudi uende nasi kupigana na Waamoni, nawe utakuwa kiongozi wetu na wa wakaaji wote wa Gileadi.” Yefuta akawaambia hao wazee wa Gileadi: “Kama mukinirudisha kwetu kwa kupigana na Waamoni halafu Yawe akiwatia katika mikono yangu, mimi nitakuwa kiongozi wenu.” Wale wazee wa Gileadi wakamwambia Yefuta: “Yawe atakuwa mushuhuda kati yetu. Hakika tutafanya kama ulivyosema.” Yefuta akafuatana na wazee wa Gileadi, nao watu wakamufanya kiongozi wao. Yefuta akasema masharti yake kule Misipa mbele ya Yawe. Yefuta akapeleka ujumbe kwa mufalme wa Amoni akamwambia: “Kuna maneno gani kati yako nasi hata ukuje kuishambulia inchi yetu?” Mufalme wa Amoni akawajibu hao wajumbe: “Waisraeli walipotoka Misri, walitwaa inchi yangu kutoka muto Arnoni mpaka kwenye muto Yaboki na muto Yordani. Sasa munirudishie inchi hiyo kwa amani.” Yefuta akatuma tena wajumbe kwa mufalme wa Amoni wamwambie kwa jina lake: “Waisraeli hawakutwaa inchi ya Wamoabu wala inchi ya Waamoni. Lakini Waisraeli walipotoka Misri, walisafiri katika jangwa mpaka kwenye bahari Nyekundu na kufika Kadesi. Kisha Waisraeli wakatuma wajumbe kwa mufalme wa Edomu wakimwomba awaruhusu kupita katika inchi yake, lakini mufalme wa Edomu akakataa. Basi wakamwomba mufalme wa Moabu ruhusa naye vilevile akakataa. Kwa hiyo Waisraeli wakabaki Kadesi. Kisha wakasafiri wakipitia katika jangwa kuzunguka inchi ya Edomu na Moabu mpaka walipofika upande wa mashariki wa Moabu, wakapiga kambi ngambo ya muto Arnoni. Lakini hawakuingia katika eneo la Moabu. Muto Arnoni ndio uliokuwa mupaka wa Moabu. Hapo Waisraeli wakatuma wajumbe kwa mufalme Sihoni wa Waamori kule Hesiboni, wakamwomba awaruhusu kupita katika inchi yake waende katika inchi yao. Lakini Sihoni hakuwakubali Waisraeli wapite katika inchi yake. Basi, Sihoni akakusanya watu wake wote, akapiga kambi kule Yahasa, akawashambulia Waisraeli. Naye Yawe, Mungu wa Israeli, akamutia Sihoni pamoja na watu wake katika mikono ya Waisraeli, wakawashinda. Hivyo Waisraeli wakatwaa inchi yote ya Waamori ambao walikuwa wanaishi kule. Walilitwaa eneo lote la Waamori tangu muto Arnoni mpaka kwenye muto Yaboki na tangu katika jangwa upande wa mashariki mpaka kwenye muto Yordani upande wa magaribi. Kwa hiyo, Yawe, Mungu wa Israeli, akawafukuza Waamori mbele ya Waisraeli. Sasa, wewe unataka kutunyanganya inchi yetu? Tosheka na kile ambacho mungu wako Kemosi amekupa. Lakini inchi yoyote ambayo Yawe, Mungu wetu, amewafukuza wakaaji wake, akatupa sisi, hiyo ni mali yetu sisi. Unazani wewe una nguvu kuliko Balaki mwana wa Sipori aliyekuwa mufalme wa Moabu? Yeye hakushindana na Waisraeli au kupigana nao. Wakati wote Waisraeli walipoishi katika muji wa Hesiboni na vijiji vyake, na muji wa Aroeri na vijiji vyake pamoja na miji yote inayokuwa kwa ukingo wa muto Arnoni kwa muda wa miaka mia tatu, kwa nini haukulikomboa eneo hilo wakati huo? Mimi sijakukosea kitu na ndiyo maana unafanya kosa unaponishambulia. Yawe ambaye ndiye Mwamuzi ataamua leo hii kati ya Waisraeli na watu wa Amoni.” Lakini mufalme wa Amoni akazarau ujumbe ule wa Yefuta. Kisha roho wa Yawe akamujaza Yefuta, naye akaondoka na kupitia Gileadi na Manase, akarudi Misipa katika inchi ya Gileadi na kuendelea mpaka Amoni. Yefuta akamwapia Yawe akisema: “Kama utawatia Waamoni katika mikono yangu, basi, yeyote atakayetoka inje kutoka katika nyumba yangu kuja kunipokea nitakapokuwa ninarudi nyuma ya kuwashinda Waamoni, huyo atakuwa wako wewe Yawe. Nitakutolea kama sadaka ya kuteketezwa.” Basi, Yefuta akavuka muto, akapigana na Waamoni, naye Yawe akawatia Waamoni katika mikono yake. Akajipatia ushindi mukubwa, akateka maeneo makumi mbili yaliyokuwa kati ya Aroeri, sehemu zilizozunguka Miniti na Abeli-Keramimu. Basi Waamoni wakashindwa kabisa na Waisraeli. Yefuta alipokuwa anarudi kwake kule Misipa, binti yake akatoka kuja kumupokea akicheza na kupiga matari. Binti huyo alikuwa ndiye mutoto wake wa pekee. Yefuta hakukuwa na mutoto mwingine mwanaume wala mwanamuke. Yefuta alipomwona, akapasua nguo yake kwa huzuni na kusema: “Ee binti yangu! Umenivunja moyo. Wewe umekuwa chanzo kikubwa cha matatizo kwangu. Nimekwisha kumwapia Yawe nami siwezi kuvunja kiapo changu.” Naye akamwambia: “Baba, kama umemwapia Yawe kitu, basi unitendee kama ulivyoahidi, kwa vile sasa amekuwezesha kuwalipiza kisasi waadui zako Waamoni.” Kisha, akamwambia baba yake: “Ninakuomba jambo hili moja, unipatie muda wa miezi miwili, niende na warafiki zangu kwenye milima, niomboleze kifo changu mbele ya kuolewa.” Baba yake akamuruhusu aende kule kwa miezi miwili. Naye akaenda pamoja na warafiki zake, wakaomboleza kufa kwake mbele ya kuolewa. Nyuma ya miezi miwili akarudi kwao. Kisha baba yake akamutendea kulingana na kiapo chake. Binti huyo hakukuwa amemujua mwanaume yeyote. Basi, tangu wakati ule kukakuwa desturi hii katika Israeli: Kila mwaka wanawake wa Israeli wanaenda kuomboleza kwa siku ine kifo cha binti ya Yefuta wa Gileadi. Watu wa kabila la Efuraimu wakakusanyika, wakavuka muto Yordani wakafika kule Safoni. Kisha wakamwambia Yefuta: “Kwa nini haukutuita tuende pamoja nawe kupigana na Waamoni? Sasa tutaichoma nyumba yako nawe mwenyewe ndani yake.” Yefuta akawaambia: “Mimi pamoja na watu wangu tulikuwa na uadui mukubwa na Waamoni. Niliwaomba munisaidie lakini hamukukuja kuniokoa. Nilipoona kwamba hamukukuja kuniokoa, nikahatarisha maisha yangu, nikavuka kwenda kupigana na Waamoni, naye Yawe akawatia katika mikono yangu. Kwa nini sasa munakuja kupigana na mimi?” Basi, Yefuta akakusanya watu wote wa Gileadi, akapigana na watu wa Efuraimu. Watu wa Gileadi wakawashinda watu wa Efuraimu. Hawa Waefuraimu ndio hao waliokuwa wamesema: “Ninyi watu wa Gileadi ni wakimbizi wa kabila la Efuraimu muliotoka katika kabila la Efuraimu mukaenda kwa kabila la Manase.” Kisha watu wakavishika vivuko vya muto Yordani kwa kuiziba njia ya watu wa Efuraimu. Kila mara mukimbizi alipotokea akiomba kupita kule, watu wa Gileadi walimwuliza: “Wewe ni Mwefuraimu?” Na kama akijibu “Hapana”, walimwambia: “Basi useme neno ‘Shiboleti’ ”. Lakini yeye akisema “Siboleti” kwa sababu hakuweza kulitamka sawasawa, walimukamata na kumwua kule kwenye vivuko vya muto Yordani. Watu elfu makumi ine na mbili wa Efuraimu wakapoteza maisha yao wakati ule. Yefuta alikuwa mwamuzi katika Israeli kwa miaka sita. Kisha akakufa, akazikwa kule Gileadi katika muji wake. Nyuma ya Yefuta, Ibusani wa muji wa Betelehemu akakuwa mwamuzi wa Israeli. Yeye alikuwa na wana makumi tatu na wabinti makumi tatu. Nao wabinti zake aliwaoesha inje ya ukoo wake, na wana aliwaoea wabinti makumi tatu kutoka inje ya ukoo wake. Ibusani alikuwa mwamuzi wa Israeli kwa miaka saba. Akakufa, akazikwa katika muji wa Betelehemu. Nyuma ya Ibusani, Eloni wa kabila la Zebuluni, akakuwa mwamuzi wa Israeli kwa miaka kumi. Naye akakufa, akazikwa katika muji wa Ayaloni katika inchi ya kabila la Zebuluni. Nyuma ya Eloni, Abudoni mwana wa Hileli wa muji wa Piratoni akakuwa mwamuzi wa Israeli. Yeye alikuwa na watoto wanaume makumi ine na wajukuu makumi tatu ambao walipanda juu ya punda makumi saba. Alikuwa mwamuzi wa Israeli kwa miaka minane. Kisha Abudoni akakufa, akazikwa katika muji wa Piratoni katika inchi ya kabila la Efuraimu kwenye eneo la milima ya Waamaleki. Waisraeli walitenda tena uovu mbele ya Yawe, naye akawaacha watawaliwe na Wafilistini kwa miaka makumi ine. Kulikuwa mutu mumoja kule Zora, wa kabila la Dani, jina lake Manoa. Muke wake alikuwa tasa. Siku moja, malaika wa Yawe akamutokea yule mwanamuke, akamwambia: “Wewe ni tasa, hauna watoto. Lakini utapata mimba na kumuzaa mutoto mwanaume. Kwa hiyo ukuwe mwangalifu, usikunywe divai au kileo wala usikule kitu chochote kinachohesabiwa kuwa kichafu, kwa maana utabeba mimba na kuzaa mutoto mwanaume. Nywele za mutoto huyo zisinyolewe hata kidogo, maana atakuwa Munaziri wa Mungu tangu kuzaliwa kwake. Naye ataanza kuwakomboa Waisraeli toka katika mikono ya Wafilistini.” Mwanamuke huyo akaenda kumwambia mume wake: “Mutu wa Mungu ambaye sura yake ilikuwa kama ya malaika wa Mungu alinitokea. Sikumwuliza anatoka wapi wala hakuniambia jina lake. Lakini aliniambia kwamba nitabeba mimba na kuzaa mutoto mwanaume. Aliniamuru nisikunywe divai au kileo wala kula chochote kinachohesabiwa kuwa kichafu, maana mutoto huyo atakuwa Munaziri wa Mungu tangu kuzaliwa kwake mpaka atakapokufa.” Kisha Manoa akamwomba Yawe, akisema: “Ninakuomba, ee Yawe, umutume tena yule mutu wako uliyemutuma kusudi atufundishe mambo tunayopaswa kumutendea huyo mutoto atakayezaliwa.” Yawe akalisikia ombi la Manoa, na yule malaika wa Mungu akamwendea tena yule mwanamuke alipokuwa akiikaa katika shamba. Lakini mume wake Manoa hakukuwa pamoja naye. Mwanamuke akakimbia upesi, akamwambia mume wake: “Yule mutu aliyenijia siku ile amenitokea tena.” Manoa akafuatana naye mpaka kwa mutu huyo, akamwuliza: “Wewe ni yule mutu aliyezungumuza na mwanamuke huyu?” Yule mutu akamujibu: “Ni mimi.” Kisha Manoa akasema: “Sasa maneno yako yatakapotimia ni mambo gani tutakayofuata kwa ajili ya huyo mutoto? Tutafanya nini kwa ajili yake?” Malaika wa Yawe akamwambia Manoa: “Muke wako atapaswa kushika yote niliyomwambia: asionje mazao yoyote ya muzabibu, wala asikunywe divai au kileo wala kula chochote kinachohesabiwa kuwa kichafu. Yote niliyomwamuru, ayafuate.” Manoa akamwambia huyo malaika wa Yawe: “Tafazali, ukae kidogo tukutayarishie mwana-mbuzi.” Yule malaika wa Yawe akamwambia Manoa: “Hata kama mukinilazimisha kukaa, sitakula chakula chenu. Lakini kama ukipenda, tayarisha sadaka ya kuteketezwa kwa moto, umutolee Yawe.” Manoa hakujua kwamba huyo alikuwa malaika wa Yawe. Basi, Manoa akamwambia huyo malaika wa Yawe: “Utuambie jina lako kusudi tukuheshimu wakati maneno yako yatakapotimia.” Malaika wa Yawe akamujibu: “Kwa nini unataka kujua jina langu? Ni la ajabu.” Hapo Manoa akatayarisha mwana-mbuzi na sadaka, akaviweka juu ya jiwe apate kumutolea Yawe anayefanya maajabu. Basi wakati Manoa na muke wake walipokuwa wanaangalia ndimi za moto zikipanda juu mbinguni kutoka kwenye mazabahu, wakamwona malaika katika ndimi hizo akipanda kwenda mbinguni. Basi Manoa na muke wake wakainama uso mpaka chini. Manoa akajua kwamba huyo alikuwa malaika wa Yawe. Malaika hakumutokea tena Manoa na muke wake. Basi, Manoa akamwambia muke wake: “Hakika tutakufa, maana tumemwona Mungu.” Lakini muke wake akamujibu: “Kama Yawe angetaka kutuua hangepokea sadaka yetu ya kuteketezwa kwa moto na ya ngano; wala hangetuonyesha mambo hayo wala kutuambia maagizo.” Kisha muke wa Manoa akazaa mutoto mwanaume, naye Manoa akamupa jina la Samusoni. Mutoto huyo akakomaa naye Yawe akamubariki. Roho wa Yawe akaanza kumusukuma akiwa kule Mahane-Dani, kati ya muji wa Zora na wa Estaoli. Siku moja, Samusoni aliteremuka na kwenda Timuna ambako alimwona binti mumoja Mufilistini. Aliporudi kwa nyumba akawaambia wazazi wake: “Nimemwona binti mumoja Mufilistini kule Timuna. Munioee binti huyo.” Lakini wazazi wake wakamwambia: “Hakuna binti yeyote kati ya wandugu zako au kati ya watu wetu kusudi uende kuoa kwa Wafilistini wasiotahiriwa?” Lakini Samusoni akamwambia baba yake: “Munioee binti huyo, maana ananipendeza sana.” Wazazi wake hawakujua kwamba ule ulikuwa mupango wa Yawe ambaye alikuwa anatafuta njia ya kushambulia Wafilistini. Wakati ule, Wafilistini walikuwa wakiwatawala Waisraeli. Samusoni na wazazi wake wakaondoka kwenda Timuna. Walipofika kule kwenye mashamba ya mizabibu, simba mukali mumoja akatokea akamungurumia Samusoni. Basi, roho wa Yawe akamushika Samusoni kwa nguvu, akamurarua simba huyo kama mutu anavyorarua mwana-mbuzi. Naye Samusoni hakuwaambia wazazi wake jambo lile. Kisha akateremuka akaenda kuzungumuza na yule binti. Yule binti alimupendeza sana Samusoni. Nyuma ya siku chache akarudi kule Timuna kwa kumutwaa yule binti. Alipokuwa katika njia akageuka pembeni kwa kuangalia muzoga wa yule simba, kumbe kulikuwa nyuki na asali ndani ya muzoga. Basi, akapakua asali kwa mikono yake, akaikula akiendelea na safari yake. Aliporudi kwa wazazi wake, akawapa asali kidogo nao wakakula. Lakini hakuwaambia kwamba alitosha asali hiyo ndani ya muzoga wa simba. Baba yake akaenda katika nyumba ya yule binti, naye Samusoni akafanya karamu kule, kama vile vijana walivyofanya kwa wakati ule. Wafilistini walipomwona Samusoni wakamuletea vijana makumi tatu wakae naye. Samusoni akawaambia: “Nitatega kitendawili. Kama mukiweza kutegua kitendawili hicho kwa muda wa siku saba za sherehe za arusi, basi, nitawapa nguo makumi tatu za kitani na nguo makumi tatu za sikukuu. Lakini musipoweza kukitegua, ninyi mutanipa nguo makumi tatu za kitani na nguo makumi tatu za sikukuu.” Nao wakamwambia: “Sasa tega tusikie.” Samusoni akawaambia: “Katika mwenye kula kukatoka chakula na katika mwenye nguvu kukatoka utamu.” Nyuma ya siku tatu hao vijana walikuwa bado hawajaweza kutegua hicho kitendawili. Basi siku ya ine wakamwambia muke wa Samusoni: “Umubembeleze mume wako kusudi atuambie maana ya kitendawili hicho, kama sivyo tutakuteketeza kwa moto wewe pamoja na nyumba ya baba yako. Ninyi mulitualika hapa kutunyanganya mali zetu?” Muke wa Samusoni akamwendea Samusoni, na machozi yakimutiririka, akamwambia: “Kwa kweli unanichukia; haunipendi hata kidogo. Umewategea kitendawili watu wangu na haukuniambia maana yake.” Samusoni akamujibu: “Mimi sijawaelezea hata wazazi wangu. Sasa nitaweza namna gani kukuelezea wewe?” Lakini aliendelea kulia katika muda wao wote wa siku saba za sherehe za arusi. Siku ya saba Samusoni akamwambia muke wake kile kitendawili kwa sababu alimwuzi sana. Muke wake akaenda haraka akawaambia watu wake. Siku hiyo ya saba, mbele ya jua kutua, wakamwambia Samusoni, “Ni kitu gani kitamu kuliko asali? Ni nani mwenye nguvu kuliko simba?” Samusoni akawajibu: “Kama hamungejishugulisha na mwana-ngombe wangu hamungeweza kukitegua kitendawili changu.” Hapo roho wa Yawe akamushika Samusoni kwa nguvu, naye akaenda muji Askeloni, akawaua watu makumi tatu, kisha akatwaa nguo zao za sikukuu, akawapa wale waliotegua kitendawili chake. Halafu akaondoka, akaenda kwa nyumba kwa wazazi wake akiwa na hasira kali. Basi, wakamwoesha mwanamuke wake kwa kijana mumoja ambaye alikuwa rafiki ya Samusoni katika arusi. Nyuma ya muda fulani, wakati wa mavuno ya ngano, Samusoni akatwaa mwana-mbuzi, akaenda kumutembelea muke wake. Akamwambia baba mukwe wake kwamba anataka kumwona muke wake ndani ya chumba chake. Lakini baba mukwe hakumuruhusu, akamwambia: “Mimi nilizani kwamba ulimuchukia kabisa. Kwa hiyo nilimwoesha kwa rafiki yako. Hata hivyo, dada yake mudogo ni muzuri kuliko yeye. Tafazali, umwoe huyo kwa pahali pake.” Samusoni akamwambia: “Mara hii sitakuwa na kosa kwa yale nitakayowatendea Wafilistini.” Basi, Samusoni akaenda, akawakamata mbweha mia tatu naye akawafunga mikia yao pamoja wawili wawili. Kisha akaweka mwenge katika kila mbweha wawili wawili. Halafu akaiwasha hiyo mienge na kuwaachilia. Wakaingia kwenye mashamba ya Wafilistini na kuteketeza miganda ya ngano na vilevile ngano iliyokuwa bado haijavunwa hata na mashamba ya mizeituni. Wafilistini walipotaka kujua aliyefanya hayo, waliambiwa: “Ni huyo Samusoni, mukwe wa Mutimuna, ndiye amefanya hivyo kwa sababu huyo baba mukwe wake ametwaa muke wake na kumwoesha kwa kijana mumoja aliyekuwa rafiki ya Samusoni mwenyewe katika arusi.” Basi Wafilistini wakaenda kumuchoma kwa moto yule mwanamuke pamoja na baba yake. Samusoni akawaambia hao Wafilistini: “Kama hayo ndiyo muliyofanya, ninaapa kwamba sitaondoka mpaka nimelipiza kisasi.” Basi, akawashambulia vikali na kuwaua wengi. Kisha akaenda kuishi katika pango la Etamu lililokuwa chini ya jiwe. Wafilistini wakakuja, wakapiga kambi yao katika inchi ya Yuda na kuushambulia muji wa Lehi. Watu wa Yuda wakawauliza: “Kwa nini mumekuja kutushambulia?” Nao wakawajibu: “Tumekuja kusudi tumufunge Samusoni na kumutendea kama alivyotutendea.” Basi, watu elfu tatu wa Yuda wakamwendea Samusoni katika pango chini ya jiwe la Etamu wakamwambia: “Haujui kwamba Wafilistini wanatawala juu yetu? Angalia basi, jambo ulilotutendea!” Samusoni akawajibu: “Kama walivyonitendea ndivyo nilivyowatendea.” Wakamwambia: “Tumekuja kukufunga kusudi tukutie katika mikono yao.” Samusoni akawaambia: “Muniapie kwamba ninyi wenyewe hamutaniua.” Nao wakamwambia: “Sisi hatutakuua lakini tutakufunga tu na kukutia katika mikono yao.” Basi, wakamufunga kwa kamba mbili mupya na kumutosha inje ya pango. Alipofika Lehi, Wafilistini wakamwendea mbio na walikuwa wanapiga kelele. Kwa rafla roho wa Yawe akamushika Samusoni kwa nguvu na zile kamba walizomufunga kwenye mikono yake zikakatika kama kitani kilichoguswa na moto, navyo vifungo vikaanguka chini. Samusoni akaona mufupa mubichi wa taya ya punda, akautumia kuwaua watu elfu moja. Kisha Samusoni akasema: “Kwa utaya wa punda, nimeua watu elfu moja. Kwa utaya wa punda, nimekusanya malundo ya maiti.” Alipomaliza kusema, akatupa utaya huo. Pahali pale pakaitwa Ramati-Lehi, maana yake “Mulima wa Utaya”. Kisha Samusoni akashikwa na kiu sana. Basi, akamwomba Yawe, akisema: “Ee Mungu, wewe ndiwe uliyeleta ukombozi huu, kwa kunitumia mimi mutumishi wako. Sasa utaniacha nikufe kwa kiu na kutekwa na Wafilistini hawa wasiotahiriwa?” Mungu akafungua pahali palipokuwa shimo kule Lehi, akatiririsha maji. Samusoni akakunywa maji hayo na nguvu zake zikamurudilia. Chemichemi hiyo ikaitwa “Kisima cha Yule Anayeita” nayo iko kule Lehi mpaka leo. Samusoni akakuwa mwamuzi wa Waisraeli kwa miaka makumi mbili, nyakati za Wafilistini. Siku moja Samusoni akakwenda katika muji wa Gaza, akakutana na kahaba mumoja akalala naye. Watu wa Gaza walipoambiwa kwamba Samusoni yuko kule, wakalizunguka eneo hilo na kumuvizia kwenye mulango wa muji usiku kucha. Wakakaa kimya kule kwenye mulango usiku wote wakifikiri kwamba wanaweza kungojea mpaka mapambazuko wapate kumwua. Lakini Samusoni akabaki katika muji mpaka saa za usiku kati. Wakati wa usiku kati akaamuka akashika miimo miwili ya mulango, akaiongoa pamoja na vifungio vyake akaibeba na kwenda nayo mpaka karibu na Hebroni. Nyuma ya mambo hayo, Samusoni akamupenda mwanamuke mumoja aliyeitwa Delila ambaye aliishi katika bonde la Soreki. Wakubwa wa Wafilistini wakamwendea Delila, wakamwambia: “Umubembeleze Samusoni kusudi ujue asili ya nguvu zake nyingi kusudi tuweze kumukamata na kumufunga. Ukifanya hivyo, kila mumoja wetu atakupa vikoroti makumi tatu vya feza.” Delila akamwambia Samusoni: “Tafazali, uniambie asili ya nguvu zako, na jinsi gani mutu anaweza kukushinda na kukufunga.” Samusoni akamujibu: “Wakinifunga kwa kamba saba mbichi za upinde, nitakuwa zaifu kama mutu yeyote.” Wakubwa wa Wafilistini wakamuletea Delila kamba hizo saba mbichi za upinde, naye akamufunga Samusoni kwa kamba hizo. Delila alikuwa ameweka watu wamuvizie katika chumba cha ndani. Kisha, akamwambia Samusoni kwa sauti kubwa: “Samusoni! Wafilistini wanafika kukushambulia.” Samusoni akazikata kamba hizo kama nyuzi za kitani zinapogusa moto. Hivyo hakuna aliyegundua siri ya nguvu zake. Delila akamwambia Samusoni: “Wewe umenichekelea. Umenidanganya. Tafazali, uniambie jinsi unavyoweza kufungwa.” Samusoni akamujibu: “Wakinifunga kwa kamba nyipya ambazo hazijatumiwa, nitakuwa zaifu kama mutu yeyote.” Basi, Delila akatwaa kamba nyipya, akamufunga nazo. Kisha akamwambia Samusoni kwa sauti kubwa: “Samusoni! Wafilistini wanakuja kukushambulia!” Wakati ule kulikuwa watu ndani ya chumba wakimuvizia. Samusoni akazikata kamba hizo kama uzi. Delila akamwambia Samusoni: “Mpaka sasa ungali unanichekelea. Umenidanganya. Uniambie namna wanavyoweza kukufunga.” Samusoni akamwambia: “Ukisuka nywele zangu kwa misuko saba na nyuzi ukitumia chombo cha kufuma nguo na kuvikaza kabisa kwa musumari, nitakuwa zaifu kama mutu yeyote.” Wakati Samusoni alipokuwa analala Delila akasuka nywele za Samusoni kwa misuko saba na nyuzi, akazifunga kwa chombo cha kufuma nguo na kukaza kabisa kwenye musumari. Kisha akamwambia Samusoni: “Samusoni! Wafilistini wanakuja kukushambulia.” Samusoni akaamuka kutoka katika usingizi akauongoa ule musumari na kutatua kile chombo cha kufuma nguo. Delila akamwambia Samusoni: “Unaweza namna gani kusema kwamba unanipenda na moyo wako hauko pamoja nami? Umenichekelea sasa mara tatu. Haujaniambia asili ya nguvu zako iko wapi.” Delila alipoendelea kumusumbua sana Samusoni kwa maneno, siku kwa siku na kumwuzi hata akachoka ndani ya roho karibu kufa, hakuweza kuvumilia, akamufunulia siri yake, akisema: “Nywele zangu hazijapata kunyolewa hata kidogo. Mimi nimewekwa Munaziri wa Mungu tangu katika tumbo la mama yangu. Kama nikinyolewa nguvu zangu zitanitoka, nami nitakuwa zaifu kama mutu yeyote.” Basi, Delila alipoona kwamba Samusoni amemwambia siri yake yote, akawaita wakubwa wa Wafilistini, akawaambia: “Mukuje mara hii moja tu maana Samusoni ameniambia siri yake yote.” Wakubwa wa Wafilistini wakamwendea Delila na walikuwa wanamuletea feza walizomwahidi. Naye Delila akamufanya Samusoni alale usingizi juu ya magoti yake, akamwita mutu amunyoe ile misuko yake saba. Kisha Delila akaanza kumutesa Samusoni kwa sababu sasa nguvu zilikuwa zimemutoka. Delila akamwambia Samusoni: “Samusoni! Wafilistini wanakuja kukushambulia!” Samusoni akaamuka toka katika usingizi naye akifikiri kwamba atatoka na kujiokoa kama vile mbele. Kumbe hakujua kwamba Yawe alikuwa amemwacha. Wafilistini wakamukamata, wakamwongoa macho, wakamupeleka Gaza, wakamufunga kwa minyororo ya shaba, na kumulazimisha kufanya kazi ya kusaga unga kule katika kifungo. Lakini nywele zake zikaanza kuota tena nyuma ya kunyolewa. Wakubwa wa Wafilistini wakakusanyika kwa kusherehekea na kumutolea mungu wao anayeitwa Dagoni sadaka. Basi, wakakuwa wanaimba: “Mungu wetu amemutia adui yetu Samusoni katika mikono yetu.” Watu walipomwona Samusoni wakamusifu mungu wao na kusema: “Mungu wetu amemutia adui yetu katika mikono yetu ambaye alikuwa akiharibu inchi yetu na kuwaua wengi kati yetu.” Walipojaa na furaha sana ndani ya mioyo yao, wakasema: “Mulete Samusoni atuchekeshe.” Basi wakamutosha Samusoni katika kifungo, wakamuleta naye akawachekesha. Wakamuweka katikati ya nguzo. Samusoni akamwambia kijana aliyekuwa anamwongoza: “Uniruhusu nizipapase nguzo zinazotegemeza chumba hiki kusudi nami niziegemee.” Nyumba hiyo ilikuwa imejaa watu: wakubwa wote wa Wafilistini walikuwa mule na kwenye paa kulikuwa watu elfu tatu wanaume na wanawake, wakimutazama Samusoni akiwachekesha. Hapo Samusoni akamwomba Yawe: “Bwana wangu Yawe, ninakuomba unikumbuke. Unitie nguvu, mara hii moja tu, ee Mungu, kusudi niwalipize kisasi mara moja hii tu Wafilistini ambao waliyaongoa macho yangu mawili.” Samusoni akazishika nguzo mbili za katikati ambazo zilitegemeza uzito wote wa nyumba ile, mukono mumoja nguzo hii na mukono mwingine nguzo ya pili. Kisha akasema: “Na nikufe pamoja na Wafilistini.” Akasukuma kwa nguvu zake zote. Nyumba ikawaangukia wakubwa hao wote wa Wafilistini waliokuwa mule ndani. Wale waliouawa wakati wa kifo chake walikuwa wengi kuliko wale aliowaua wakati alipokuwa muzima. Wandugu zake na jamaa yake yote wakakuja kubeba maiti yake. Wakamuzika katikati ya muji wa Zora na muji wa Estaoli katika kaburi la Manoa, baba yake. Samusoni alikuwa mwamuzi wa Israeli kwa miaka makumi mbili. Kulikuwa mutu mumoja kule katika milima ya Efuraimu, jina lake Mika. Siku moja akamwambia mama yake: “Vile vikoroti vya feza elfu moja na mia moja ulivyoibiwa, nawe ukamulaani aliyekuiba nami nikiwa ninasikia, mimi niko navyo. Mimi ndiye niliyevibeba.” Mama yake akasema: “Mwana wangu ubarikiwe na Yawe.” Mika akamurudishia mama yake hivyo vikoroti vya feza elfu moja na mia moja. Mama yake akasema: “Kusudi laana niliyotoa isikupate, feza hii ninaitoa kwa Yawe kwa kutengeneza sanamu ya kuchonga na ya kuyeyushwa. Sasa ninakurudishia vikoroti vya feza.” Mika alipomurudishia mama yake hiyo feza, mama yake akatwaa vikoroti vya feza mia mbili akamupatia mufua feza ambaye alifua sanamu ya kuchonga na ya kuyeyushwa. Sanamu hiyo ikawekwa katika nyumba ya Mika. Mutu huyo, Mika alikuwa na pahali pake pa ibada. Alitengeneza kizibao cha kuhani na sanamu, kisha akamufanya mumoja wa watoto wake kuwa kuhani wake. Siku hizo hakukukuwa mufalme katika Israeli. Kila mutu alifanya chochote alichotaka. Wakati ule kulikuwa kijana mumoja Mulawi katika muji wa Betelehemu katika inchi ya Yuda. Kijana huyo akaondoka Betelehemu katika inchi ya Yuda, akaenda kutafuta pahali pengine pa kuishi. Katika safari yake akafika katika nyumba ya Mika katika inchi ya milima ya Efuraimu. Mika akamwuliza: “Umetoka wapi?” Naye akamujibu: “Mimi ni Mulawi, kutoka katika muji wa Betelehemu katika inchi ya Yuda. Nitakaa popote nitakapopata nafasi ya kukaa kama mugeni.” Mika akamwambia: “Kaa pamoja nami, ukuwe kwangu kama baba na kuhani wangu. Nitakulipa vikoroti kumi vya feza kila mwaka na nguo pamoja na mahitaji yako.” Yule Mulawi akakubali, akakaa kule na kuwa kama mumoja wa wana wa Mika. Naye Mika akamufanya kijana huyo Mulawi kuwa kuhani wake kule katika nyumba yake. Kisha akasema: “Sasa ninajua kwamba Yawe atanifanikisha maana nina kijana huyu Mulawi kama kuhani wangu.” Katika siku zile hakukukuwa mufalme katika Israeli. Basi kabila la Dani lilikuwa linatafuta eneo lake lenyewe la kuishi ndani yake, maana mpaka wakati ule, halikukuwa limegawanyiwa sehemu yake lenyewe kati ya makabila ya Israeli. Kwa hiyo watu wa kabila la Dani wakachagua kati yao watu hodari, wakawatuma kutoka kule Estaoli na Zora, wakawaamuru waende kuipeleleza inchi. Basi watu hao wakafika katika inchi ya milima ya Efuraimu katika nyumba ya Mika, wakaenda na kukaa mule. Walipokuwa kwa Mika, wakaitambua sauti ya yule kijana Mulawi. Wakamugeukia na kumwuliza: “Nani amekuleta huku? Una shuguli gani hapa?” Yeye akawajibu: “Mika amefanya nami mupango. Amenipa kazi nami nimekuwa kuhani wake.” Nao wakamwambia: “Tafazali utuulizie kwa Yawe kama tutafanikiwa katika safari yetu.” Yule kuhani akawaambia: “Muende kwa amani. Yawe anaichunga safari yenu.” Basi, watu hao watano wakaondoka, wakaenda Laisi. Waliwaona watu walioishi kule, na jinsi walivyokaa kwa usalama kama vile watu wa Sidona. Walikuwa watu watulivu wasiokuwa na wasiwasi na hawakupungukiwa mahitaji yoyote katika inchi. Walikuwa mbali na watu wa Sidona, na hawakukuwa na shuguli yoyote na watu wengine. Basi hao wapelelezi wakarudi kwa wandugu zao huko Zora na Estaoli, nao wakawauliza: “Mumetuletea habari gani?” Wao wakasema: “Musimame tuende na kuishambulia inchi hiyo. Tumeiona na kweli ni inchi yenye mboleo. Mutakaa hapa tu bila kufanya kitu? Musikawie kwenda kuirizi inchi hiyo. Mutakapofika kule mutakuta watu wasiokuwa na wasiwasi wowote. Inchi hiyo ni kubwa, haikupungukiwa chochote, na Mungu ameitia katika mikono yetu.” Basi, watu mia sita wa kabila la Dani wakiwa na silaha zao za vita wakaondoka kutoka Zora na Estaoli, wakaenda kupiga kambi yao kule Kiriati-Yearimu katika inchi ya Yuda. Ndiyo maana pahali pale, upande wa magaribi wa Kiriati-Yearimu pameitwa Kambi ya Dani mpaka leo. Kutoka kule wakaelekea inchi ya milima ya Efuraimu, wakafika katika nyumba ya Mika. Watu wale watano waliokwenda kuipeleleza inchi ya Laisi wakawaambia wandugu zao: “Munajua kwamba katika nyumba moja kati ya hizi kuna kizibao, sanamu ya kuchongwa na sanamu yenye kuyeyushwa? Basi, mufikiri namna ya kufanya.” Basi wale wapelelezi wakaelekea kwenye nyumba ya Mika, wakaingia ndani na kumwuliza habari za yule kijana Mulawi. Wakati ule, wale watu mia sita wa kabila la Dani wakiwa na silaha zao za vita wakasimama kwenye mulango. Wale watu watano waliokwenda kuipeleleza inchi wakaingia ndani, wakabeba ile sanamu ya mungu yenye kuyeyushwa, kile kizibao na sanamu ya ibada. Wakati ule yule kuhani alikuwa akisimama kwenye mulango pamoja na wale watu mia sita wenye silaha. Basi, alipowaona wale wapelelezi wanaingia ndani ya nyumba ya Mika na kutwaa sanamu ya kuchonga, kifuko cha kuomba shauri, sanamu ya kuchongwa na sanamu ile yenye kuyeyushwa, akawauliza: “Munafanya nini?” Nao wakamwambia: “Nyamaza, funga kinywa chako, ukuje pamoja nasi, ukuwe kuhani wetu na kama baba yetu. Au unaona namna gani? Inafaa kwako zaidi kuwa kuhani wa mutu mumoja au kuwa kuhani wa kabila moja la Israeli?” Yule kuhani akafurahi sana akatwaa kile kifuko, ile sanamu ya ibada, na ile sanamu ya mungu yenye kuyeyushwa, akafuatana nao. Basi, wakaanza safari yao, na walikuwa wanatanguliwa na watoto wao na nyama wao na mali zao. Walipokuwa wamefika mbali na nyumba ya Mika, watu waliokuwa jirani na Mika wakaitwa, wakawafuatilia watu wa kabila la Dani, wakawafikia. Kisha wakawapigia kelele, nao watu wa kabila la Dani wakageuka, wakamwuliza Mika: “Una shida gani hata umetufuatilia pamoja na kundi hili lote?” Mika akasema: “Ninyi mumebeba miungu yangu niliyojitengenezea, mukamutwaa na kuhani wangu, mukaniacha bila kitu chochote. Munaweza namna gani basi kuniuliza nina shida gani?” Watu wa kabila la Dani wakamwambia: “Afazali uache kelele zako, kama sivyo wengine wetu wenye hasira wanaweza kukushambulia, nawe utapoteza maisha yako na maisha ya jamaa yako.” Mika alipoona kwamba wamemuzidia nguvu, akageuka, akarudi kwake; nao watu wa kabila la Dani wakaenda zao. Hao watu wa kabila la Dani walivitwaa vitu vile ambavyo Mika alikuwa amevitengeneza, na kumupeleka yule kuhani aliyemutumikia. Basi wakaenda kushambulia muji wa Laisi, wakawaua wakaaji wake ambao waliishi mule kwa utulivu na bila wasiwasi, wakauteketeza muji ule. Wakaaji wa muji ule hawakukuwa na mutu wa kuwaokoa kwa sababu walikuwa mbali na muji wa Sidona, tena hawakukuwa na ushirika na watu wengine. Muji ule ulikuwa kwenye bonde la Beti-Rehobu. Watu wa kabila la Dani wakaujenga upya, wakaishi mule. Walibadilisha jina la muji ule, wakauita Dani, kufuata jina la babu yao aliyekuwa mwana wa Israeli. Lakini muji ule pale mbele uliitwa Laisi. Watu wa kabila la Dani wakaisimika ile sanamu ya kuchonga, naye Yonatani mwana wa Gersoni, mujukuu wa Musa, akakuwa kuhani wao. Wazao wake vilevile walikuwa makuhani wa kabila la Dani mpaka wanainchi wa inchi hiyo walipopelekwa katika uhamisho. Wakati wote nyumba ya Mungu ilipokuwa kule Shilo, watu wa kabila la Dani waliiabudu sanamu ya kuchonga ambayo Mika aliitengeneza. Wakati ule hakukukuwa bado mufalme katika Israeli. Kulikuwa Mulawi mumoja aliyeishi kama mugeni mbali katika eneo la milima ya Efuraimu. Mutu yule alitwaa habara kutoka Betelehemu katika inchi ya Yuda. Lakini habara yule akamukasirikia yule Mulawi, akamwacha na kurudi katika nyumba ya baba yake kule Betelehemu, akakaa kwa muda wa miezi mine. Siku moja, mume wake akakwenda kumutafuta. Alikusudia kuongea naye vizuri na kumurudisha kwa nyumba yake. Akakwenda pamoja na mutumishi wake na punda wawili. Basi yule mwanamuke akamupeleka ndani kwa baba yake, naye baba mukwe alipomwona akamupokea kwa furaha. Baba mukwe akamukaribisha, naye akakaa kule kwa muda wa siku tatu. Yule Mulawi na mutumishi wake wakakula, wakakunywa na kulala kule. Siku ya ine, wakaamuka asubui mapema, wakajitayarisha kuondoka; lakini baba wa yule mwanamuke akamwambia: “Kwanza kula chakula kidogo upate nguvu, kisha uondoke.” Basi hao watu wawili wakaikaa, wakakula na kunywa pamoja. Kisha baba mukwe akamwambia: “Tafazali, ulale hapa usiku huu na kufurahi.” Yule mutu aliposimama akitaka kuondoka, baba mukwe akamusihi abaki, naye akabaki. Siku ya tano yule mutu akaamuka asubui, akataka kuondoka. Lakini baba ya yule mwanamuke akamwambia: “Kwanza upate nguvu kwa kula, ungoje mpaka jua litakaposhuka, halafu uondoke.” Basi wote wawili wakakula pamoja. Yule Mulawi na habara yake pamoja na mutumishi wake waliposimama kwenda zao, baba mukwe wake akamwambia yule Mulawi: “Sasa muchana umekwisha na magaribi imekaribia. Ulale hapa, na kufurahi. Kesho asubui utaamuka mapema kuanza safari yako ya kurudi kwako.” Lakini yule mutu akakataa kulala kule usiku ule. Basi, akasimama, akaondoka, akafika karibu na muji wa Yebusi, ni kusema Yerusalema. Alikuwa na wale punda wake wawili waliotandikwa tayari, pamoja na habara yake. Walipokuwa wanakaribia muji wa Yebusi, siku ilikuwa karibu imekwisha, naye mutumishi akamwambia bwana wake: “Sasa heri tuingie katika muji huu wa Wayebusi tulale mule usiku huu.” Bwana wake akamujibu: “Hatutageuka na kuingia katika muji wa wageni ambao si Waisraeli. Tutaendelea na safari mpaka Gibea. Tuende tukaribie sehemu hizo na kulala kule Gibea au Rama.” Basi, wakaendelea na safari yao mpaka jua likatua wakiwa karibu na muji wa Gibea ambao ni muji wa kabila la Benjamina. Wakaingia ndani ya muji wapate kulala mule usiku. Walipoingia katika muji, wakaenda kukaa kwenye kiwanja cha makutano cha muji, maana hakuna mutu aliyewakaribisha ndani ya nyumba yake. Walipokuwa kule muzee mumoja akafika kutoka kwa shamba lake. Muzee huyo alikuwa mutu wa inchi ya milima ya Efuraimu na alikuwa akiishi kule Gibea kama mugeni. Wakaaji wa muji wa Gibea walikuwa wa kabila la Benjamina. Muzee yule alipoangalia na kumwona yule musafiri akiwa kule katika kiwanja, akamwuliza: “Umetoka wapi na unakwenda wapi?” Naye akamujibu: “Tunatoka Betelehemu katika inchi ya Yuda na tunaelekea sehemu za mbali za eneo la milima ya Efuraimu. Kule ndiko ninakoishi na sasa ninarudi katika safari toka kule Betelehemu katika Yuda na kurudia kwangu; hakuna mutu hapa aliyetukaribisha katika nyumba yake. Lakini sisi watumishi wako tuna nyasi na malisho kwa ajili ya punda wetu. Vilevile nina mukate na divai; hivyo vinanitosha mimi, habara wangu na mutumishi wangu. Hatukosewi kitu chochote.” Huyo muzee akamwambia: “Amani ikuwe nanyi! Nitawapa mahitaji yote. Lakini musilale huku katika kiwanja.” Hivyo akawapeleka katika nyumba yake na kuwapa punda wao malisho. Hao wasafiri wakanawa miguu yao, wakakula na kunywa. Walipokuwa wanajifurahisha, kumbe wanaume watenda maovu wa muji ule wakakuja wakaizunguka nyumba ile na kugonga kwa mulango. Wakamwambia muzee mwenye nyumba: “Umutoshe inje yule mwanaume aliyekuja kwako, tulale naye.” Lakini yule muzee mwenye nyumba akatoka inje, akawaambia: “Sivyo wandugu zangu. Ninawasihi musitende uovu ule. Huyu ni mugeni wangu. Musimutendee ubaya ule. Ningali na binti yangu ambaye ni bikira na kuna vilevile yule habara wa mugeni wangu. Muniruhusu niwatoshe inje, muwakamate na kuwatendea kama munavyotamani, lakini mutu huyu musimutendee jambo hilo la kipumbafu.” Lakini wanaume hao hawakumusikiliza. Kwa hiyo Mulawi yule akamutwaa habara yake na kumutoa kwao kule inje. Nao wakamutwaa na kulala naye kwa kinguvu usiku kucha mpaka asubui. Karibu na mapambazuko, wakamwacha aende zake. Asubui, yule mwanamuke akakuja mpaka kwenye mulango wa nyumba ambamo bwana wake alikuwa, akaanguka chini pale kwenye mulango na kubakia pale mpaka kulipopambazuka kabisa. Bwana wa mwanamuke yule alipoamuka asubui, akafungua milango ya nyumba, akatoka inje kusudi aendelee na safari. Kwa rafla akamukuta habara yake amelala chini mbele ya mulango, mikono yake ikishika kizingiti cha mulango. Akamwambia: “Simama tuende.” Lakini yeye hakujibu kitu. Akamukamata, akamuweka juu ya punda wake na kumupeleka mpaka kwake. Alipofika kwake akatwaa kisu na kumukatakata yule habara vipande kumi na viwili. Kisha akavipeleka vipande hivyo katika maeneo yote ya inchi ya Israeli. Wale wote walioona jambo hilo wakasema: “Jambo kama hili halijatukia wala kuonekana tangu siku ile Waisraeli walipotoka katika inchi ya Misri mpaka leo. Tufikiri juu yake, tushauriane na kuamua.” Watu wote wa Israeli, kutokea Dani mpaka Beri-Seba, pamoja na watu wa inchi ya Gileadi, wakakusanyika kule Misipa, mbele ya Yawe. Viongozi wote wa makabila ya Israeli wakajitokeza mbele ya mukusanyiko wa watu wa Mungu. Wote kwa jumla walikuwa waaskari elfu mia ine wa miguu wenye silaha. Nao watu wa kabila la Benjamina, wakapata habari kwamba watu wale wengine wa Israeli walikuwa wamekusanyika kule Misipa. Basi Waisraeli wakamwuliza yule mwanaume Mulawi: “Utuelezee, uovu ule ulifanyika namna gani?” Yule Mulawi, mume wa yule muke, akawajibu: “Mimi na habara yangu tulifika katika muji wa Gibea, muji wa kabila la Benjamina kusudi tulale kule usiku. Lakini watu wa muji wa Gibea wakakuja usiku wakaizunguka nyumba nilimokuwa nimelala. Wakataka kuniua, wakamutendea kwa kinguvu habara yangu mpaka akakufa. Mimi nikabeba maiti yake, nikamukatakata vipande na kuvipeleka kwa makabila yote ya Israeli, maana wamefanya jambo la kuchukiza na potovu katika Israeli. Sasa enyi Waisraeli, mushauriane na mutoe uamuzi wenu.” Watu wote kwa pamoja, wakasimama na kusema: “Hakuna yeyote kati yetu atakayerudi katika hema yake au katika nyumba yake. Hivi ndivyo tutakavyofanya juu ya Gibea: Tutapiga kura namna ya kuwashambulia. Tutachagua watu kumi katika kila watu mia moja wa Israeli, watu mia moja katika kila watu elfu moja, watu elfu moja katika kila watu elfu kumi. Hao watakuwa na kazi ya kuwaletea chakula wenzao watakaokuwa na kazi ya kuuazibu muji wa Gibea katika inchi ya Benjamina kwa ajili ya ubaya wao na upotovu walioufanya katika Israeli.” Kwa hiyo wanaume wote wa Israeli wakakusanyika kwa moyo mumoja kwa kushambulia muji wa Gibea. Watu wa makabila ya Israeli wakatuma wajumbe mpaka kila sehemu ya kabila la Benjamina, wakisema: “Ni uovu gani huu uliotukia kati yenu? Sasa mutupe hao watu watenda maovu wa Gibea kusudi tuwaue na kuondoa uovu huu kutoka Israeli.” Lakini watu wa kabila la Benjamina hawakuwasikiliza wandugu zao, Waisraeli. Basi wakakusanyika kule Gibea kutoka katika kila muji wao, kwa kupigana na Waisraeli. Watu wa kabila la Benjamina wakakusanya kutokea miji yao jeshi la watu elfu makumi mbili na sita wenye kutumia silaha, nao wakaaji wa muji wa Gibea wakakusanya watu mia saba waliochaguliwa. Kati ya watu hao waliochaguliwa kulikuwa watu mia saba waliotumia zaidi mukono wa kushoto; kila mumoja aliweza kurusha jiwe kwa mujeledi na kupiga unywele bila kukosa. Waisraeli, bila kuhesabu kabila la Benjamina, wakakusanya watu elfu mia ine wanaozoea kutumia silaha. Wote walikuwa hodari wa vita. Waisraeli wakaenda Beteli kuomba shauri kwa Mungu, wapate kujua kabila ambalo litakwenda kwanza kupigana na watu wa kabila la Benjamina. Yawe akataja kabila la Yuda liende kwanza. Basi, Waisraeli wakaenda asubui, wakapiga kambi yao karibu na muji wa Gibea. Waisraeli wakatoka kwa kupigana na watu wa kabila la Benjamina karibu na Gibea. Watu wa kabila la Benjamina wakatoka inje ya muji wa Gibea, wakapigana na Waisraeli, wakawaangusha chini siku hiyo, watu wa Israeli elfu makumi mbili. Lakini Waisraeli wakajipa moyo, wakajipanga tena kwa vita pahali pale walipojipanga kwa mara ya kwanza. Basi Waisraeli wakaenda juu, wakamulilia Yawe mpaka magaribi. Kisha wakaomba shauri kwa Yawe: “Twende tena kupigana na wandugu zetu, wa kabila la Benjamina?” Yawe akawajibu: “Muende mupigane nao.” Hivyo, kwa siku ya pili Waisraeli wakakaribia kupigana na watu wa kabila la Benjamina. Kwa siku hiyo ya pili watu wa kabila la Benjamina walitoka Gibea na kuwashambulia Waisraeli, wakawaangusha chini Waisraeli elfu kumi na nane. Watu wote wa jeshi la Waisraeli wakaenda Beteli. Wakaikaa kule mbele ya Yawe wakiomboleza na kufunga mpaka magaribi. Wakamutolea Yawe sadaka za kuteketezwa kwa moto na sadaka za amani. Waisraeli wakamwomba Yawe awape shauri. Wakati ule Sanduku la Agano la Yawe lilikuwa kule Beteli. Finehasi mwana wa Eleazari mwana wa Haruni alikuwa na kazi ya kutumika mbele yake. Waisraeli wakamwuliza Yawe: “Twende tena kupigana na wandugu zetu, watu wa kabila la Benjamina?” Yawe akawaambia: “Muende. Kesho nitawatia katika mikono yenu.” Hivyo, Waisraeli wakaweka watu kwenye maficho kuuzunguka muji wa Gibea. Waisraeli wakaenda kupigana na watu wa kabila la Benjamina katika siku ya tatu. Wakajipanga kwa kushambulia muji wa Gibea kama walivyofanya nyakati za mbele. Kisha watu wa kabila la Benjamina walipotoka katika muji kwa kuanza kupigana na Waisraeli, walivutwa kutoka inje ya muji. Ilitokea tena kama walivyofanya nyakati za mbele. Wakawaua wamoja kati ya watu wa Israeli kwenye njia kubwa zinazoelekea miji ya Beteli na Gibea, mpaka katika mbuga. Waliua Waisraeli yapata makumi tatu. Watu wa Benjamina wakafikiri: “Tumewapiga kama nyakati zilizopita.” Lakini Waisraeli wakasema: “Sisi tukimbie kusudi tuwavute mbali na muji mpaka kwenye njia kubwa.” Hivyo watu wote wa Israeli wakatoka kwenye sehemu yao na kujipanga tena kule Bali-Tamari. Wenzao waliokuwa wanafichama wakatoka haraka pahali pao upande wa magaribi wa muji wa Gibea. Waaskari hodari waliochaguliwa kutoka makabila yote ya Israeli wakafika pale mbele ya muji wa Gibea. Vita ya siku hiyo ilikuwa kali. Lakini watu wa Benjamina hawakufahamu kwamba kuangamia kwao kulikuwa karibu. Yawe akawashinda watu wa Benjamina mbele ya Waisraeli. Waisraeli wakawaua watu wa Benjamina elfu makumi mbili na tano na mia moja. Hao wote waliouawa walikuwa waaskari walioweza kutumia silaha. Kwa hiyo watu wa kabila la Benjamina wakaona kwamba wameshindwa. Waisraeli wakarudi nyuma sawa vile wanawakimbia watu wa kabila la Benjamina, maana walitegemea wenzao waliokuwa wamewekwa kufichamia muji wa Gibea. Wale waliowekwa kufichamia muji walitoka haraka na kuushambulia muji wa Gibea na kuwaua wote waliokuwa mule kwa upanga. Walikuwa wamekubaliana na wale watu wengine wa Israeli juu ya kitambulisho kimoja. Walikubaliana kwamba wale waliokuwa wanajificha watakapoona moshi mukubwa unapanda juu kutoka katika muji, basi, wageuke kwa kupigana. Wakati ule, watu wa kabila la Benjamina walikuwa wamekwisha kuua watu yapata makumi tatu wa Israeli na kuambiana: “Tumewapiga kama pale mbele.” Lakini kile kitambulisho cha moshi kilipoanza kutokea katika muji, watu wa kabila la Benjamina wakaangalia nyuma yao, wakashangaa kuona kwamba muji wao ulikuwa unateketezwa kwa moto. Halafu Waisraeli wakageuka kwa kupigana, na watu wa kabila la Benjamina wakashikwa na woga maana sasa waliona kwamba kuangamia kwao kulikuwa kumekaribia. Wakawakimbia Waisraeli kuelekea katika jangwa, lakini vita ikawapata. Wakajikuta wako katikati ya majeshi mawili ya Israeli, na waaskari waliotoka wakawaangamiza. Waisraeli waliwazunguka watu wa kabila la Benjamina, wakawafuatilia kutoka Noha mpaka upande wa mashariki wa muji wa Gibea wakiwaua wengi kati yao. Siku hiyo watu elfu kumi na nane wa kabila la Benjamina, wote waaskari hodari, wakauawa. Watu wengine wa kabila la Benjamina wakakimbia kuelekea upande wa jangwa mpaka kwenye mulima wa Rimoni. Wengine elfu tano waliuawa kwenye njia kubwa walipokuwa wanakimbia. Waisraeli waliendelea kuwafuatilia vikali watu wa kabila la Benjamina mpaka kwenye muji wa Gidomu, wakawaua watu elfu mbili. Jumla ya watu wote wa kabila la Benjamina waliouawa siku hiyo ilikuwa elfu makumi mbili na tano, waaskari hodari wa kutumia silaha. Lakini wanaume mia sita wa kabila la Benjamina walipata kukimbilia katika jangwa mpaka kwenye mulima wa Rimoni, wakakaa kule kwa muda wa miezi mine. Waisraeli wakawageukia watu wengine wa kabila la Benjamina, wakawaua wote: wanaume, wanawake, watoto na nyama. Na miji yote waliyoikuta kule wakaiteketeza kwa moto. Waisraeli walikuwa wameapa kule Misipa kwamba hakuna hata mumoja kati yao ambaye angemwachilia binti yake aolewe kwa watu wa kabila la Benjamina. Basi, wakaenda mpaka Beteli wakakaa kule mbele ya Mungu mpaka magaribi. Wakalalamika kwa sauti na kulia kwa uchungu mwingi. Wakasema: “Ee Yawe, Mungu wa Israeli, kwa nini jambo hili limetukia hata tupungukiwe na kabila katika Israeli?” Kesho yake watu wakaamuka mapema, wakajenga mazabahu, wakatoa sadaka za kuteketezwa kwa moto na sadaka za amani. Kisha wakaulizana: “Kati ya makabila yote ya Israeli kuna kikundi chochote ambacho hakikuhuzuria mukutano uliofanyika mbele ya Yawe?” Walikuwa wamefanya kiapo kwamba mutu yeyote ambaye hatahuzuria mbele ya Yawe kule Misipa anapaswa kuuawa. Lakini Waisraeli wakawaonea huruma wandugu zao wa kabila la Benjamina, wakasema: “Leo kabila moja la Israeli limeangamia. Sasa tutafanya nini kwa kuwapatia wanawake hao wanaume wa kabila la Benjamina waliobaki kwa vile tulikwisha kuapa kwa jina la Yawe kwamba hatutawapa wabinti zetu wakuwe wake zao?” Wakataka kujua kama kulikuwa kikundi chochote cha makabila ya Israeli ambacho hakikuhuzuria mukutano mbele ya Yawe kule Mispa. Wakagundua kwamba hakuna mutu yeyote kutoka Yabesi-Gileadi aliyekuja kwenye mukutano ule. Waisraeli walipohesabiwa kule Misipa hakuna mukaaji yeyote wa Yabesi-Gileadi aliyehuzuria. Kwa hiyo Waisraeli wakapeleka watu wake elfu kumi na mbili elfu wanaokuwa hodari kabisa na kuwaamuru: “Muende muwaue wakaaji wa Yabesi-Gileadi; wanawake pamoja na watoto. Mutawaua wanaume wote na wanawake wote wasiokuwa mabikira.” Basi wakakuta kati ya wakaaji wa Yabesi-Gileadi wabinti mia ine ambao hawakukuwa wamekwisha kulala na mwanaume yeyote, wakawapeleka katika kambi kule Shilo katika inchi ya Kanana. Kisha wote pamoja wakawapelekea ujumbe wa amani watu wa kabila la Benjamina ambao walikuwa kwenye mulima wa Rimoni. Wanaume hao wa kabila la Benjamina wakawarudilia hao wenzao wakati uleule. Basi wakapewa wale wanawake ambao walikuwa wameachwa kule Yabesi-Gileadi. Lakini wanawake hao hawakuwatosha. Waisraeli wakawaonea huruma watu wa kabila la Benjamina, maana Yawe alisababisha kukuwe shimo kati ya Waisraeli. Kisha wazee wa Israeli wakasema: “Sasa tutafanya nini kwa kuwapatia wake hao wanaume waliobaki kwa vile wanawake wote wa kabila la Benjamina waliangamia? Inafaa wanaume waliobaki wa kabila la Benjamina wapewe wanawake kusudi waendeleshe kabila, na hivyo kusipotee kabila lolote katika Israeli. Lakini hatuwezi kuwatoa wabinti zetu wakuwe wake zao, maana tulikwisha kuapa kwamba mutu yeyote atakayemwoesha binti yake kwa mwanaume wa kabila la Benjamina alaaniwe.” Basi wakakumbuka kwamba sikukuu ya Yawe iliyofanyika kila mwaka kule Shilo, muji unaokuwa upande wa kaskazini wa Beteli, kwenye njia kubwa inayotoka Beteli kwenda Sekemu, ilikuwa inakaribia. Kwa hiyo wakawaamuru wale wanaume wa kabila la Benjamina: “Muende muvizie na kufichama katika mashamba ya mizabibu.” Mukuwe macho. Wabinti wa Shilo watakapotoka inje kwa kucheza wakati wa sikukuu, mutoke kwenye mizabibu na kila mutu ajikamatie binti mumoja akuwe muke wake. Kisha murudi katika inchi ya Benjamina. Baba zao au kaka zao wakikuja kutulalamikia tutawaambia: “Sisi tunawaomba muwahurumie watu wa Benjamina na kuwaacha watwae hao wanawake; maana hatukupata wanawake wa kutosha katika vita ya Yabesi-Gileadi. Na kwa sababu si ninyi wenyewe muliowapatia hao wabinti zenu, hamutahukumiwa kwamba mumevunja kiapo.” Wale wanaume wa kabila la Benjamina wakafanya hivyo, kila mumoja akajichagulia binti kati ya wabinti waliotoka inje kwa kucheza kule Shilo na kumutwaa kuwa muke wake. Kisha wakarudi katika eneo lao, wakaijenga miji yao upya na kuishi mule. Wakati uleule Waisraeli wakaondoka, kila mutu akarudi katika eneo la kabila lake na jamaa yake. Kila mutu akarudi katika sehemu aliyogawanyiwa. Siku hizo hakukukuwa mufalme katika Israeli. Kila mutu alifanya sawa vile alivyotaka. Hapo zamani, wakati waamuzi walipokuwa wanatawala Waisraeli, kulitokea njaa katika inchi. Mutu mumoja kutoka Betelehemu katika Yuda pamoja na muke wake na watoto wao wanaume wawili walikwenda kuishi kwa muda katika inchi ya Moabu kwa kuishi kama wageni. Mutu yule aliitwa Elimeleki na muke wake aliitwa Naomi. Watoto wao wawili wanaume, mumoja aliitwa Malona na mwingine Kiliona. Mutu yule na jamaa yake walikuwa wa kabila la Efuraimu kule Betelehemu katika Yuda. Walikwenda katika inchi ya Moabu, wakakaa kule. Lakini Elimeleki, mume wa Naomi, akakufa na Naomi akaachwa na wana wake. Vijana hao walioa wabinti wa Kimoabu, Orupa na Ruta. Nyuma ya miaka kumi hivi, Malona na Kiliona nao vilevile wakakufa. Kisha, Naomi akapata habari kwamba Yawe alikuwa amewabariki watu wake kwa kuwapa chakula. Basi, akaondoka kutoka Moabu kurudi kwao, pamoja na wakwe zake. Akaondoka pahali pale alipoishi pamoja na wakwe zake, wakashika njia ya kurudi Yuda. Naomi akawaambia hao wakwe zake wawili: “Murudi kila mumoja kwa mama yake. Ninaomba Yawe awatendee mema kama vile mulivyonitendea mema mimi na wale watu wangu waliokufa. Yawe awajalie, kila mumoja wenu apate mume na nyumba yake.” Kisha Naomi akawaaga kwa kuwabusu. Lakini wao walianza kulia kwa sauti na kumwambia: “Hapana hata kidogo! Tutakwenda pamoja nawe kwa watu wako.” Naye Naomi akawasihi: “Murudi, wabinti zangu. Kwa nini kunifuata? Munafikiri ninaweza kupata tena watoto watakaokuwa waume zenu? Murudi kwenu wabinti zangu, kwa maana mimi ni muzee sana, siwezi kuolewa tena. Hata kama ningesema nina tumaini, na hata kama ningepata mume usiku huu na kupata watoto, mungeweza kungoja mpaka wakomae? Mungeweza kujizuia musiolewe na wanaume wengine? Sivyo, wabinti zangu! Mambo yangu ni magumu sana kwa ajili yenu, maana Yawe amenipiga pigo.” Kwa hiyo wakalalamika wakaanza kulia tena. Halafu Orupa akamukumbatia mama mukwe wake, akamwaga na kurudi kwao. Lakini Ruta, akashikamana naye. Basi Naomi akamwambia: “Ruta, angalia dada yako amerudi kwao na kwa mungu wake; basi, nawe vilevile urudi, umufuate dada yako.” Lakini Ruta akamujibu: “Usinisihi nikuache wewe, wala usinizuie kufuatana nawe. Popote utakapokwenda ndipo nami nitakapokwenda, na pale utakapokaa mimi nitakaa, watu wako watakuwa watu wangu, na Mungu wako atakuwa Mungu wangu. Pale utakapokufia ni pale nitakufia nami, na ni palepale nitazikwa. Yawe anipe azabu kali kama nikitenganishwa nawe isipokuwa tu kwa kifo.” Naomi alipoona kwamba Ruta ameamua kwenda pamoja naye, aliacha kumushawishi. Halafu wote wawili wakaendelea na safari mpaka Betelehemu. Walipofika kule, watu wote wakashangaa, hata wanawake wakaulizana: “Huyu ni Naomi?” Naomi akasema: “Musiniite tena Naomi muniite Mara, kwa maana Mungu Mwenye Nguvu ameyafanya maisha yangu yakuwe machungu sana. Nilipoondoka hapa, nilikuwa na vitu vingi, lakini sasa Yawe amenirudisha mikono mitupu. Mbona munaniita Naomi ijapokuwa Yawe ameniazibu, naye Mungu Mwenye Nguvu amenitesa?” Hivi ndivyo Naomi pamoja na mukwe wake Ruta wa Moabu walivyorudia kutoka Moabu, na wakafika Betelehemu wakati mavuno ya shayiri yalipokuwa yanaanza. Naomi alikuwa na ndugu aliyeitwa Boazi, wa ukoo wa Elimeleki mume wake. Huyo alikuwa mutu mwenye heshima na tajiri. Siku moja, Ruta wa Moabu akamwambia Naomi: “Muniruhusu niende kukusanya masalio ya mavuno pahali nitakapopata kukubaliwa na mwenye shamba.” Naomi akamwambia: “Basi, uende binti yangu.” Basi Ruta akaenda katika shamba, akawafuata wavunaji naye akiyaokota masuke waliyoyaacha. Na kumbe akajikuta katika shamba la Boazi, yule wa ukoo wa Elimeleki. Nyuma ya muda, Boazi akafika kutoka Betelehemu, akawasalimia wavunaji, akasema: “Yawe akuwe nanyi.” Nao wakamujibu: “Yawe akubariki.” Kisha Boazi akamwuliza musimamizi wa wavunaji: “Yule binti ni nani?” Yule kiongozi wa wavunaji akajibu: “Ni binti Mumoabu aliyekuja pamoja na Naomi kutoka katika inchi ya Moabu. Aliniomba nimuruhusu awafuate nyuma wavunaji naye akiokota masalio kati ya miganda. Basi alikuja na amefanya kazi tangu asubui na ni sasa tu amekwenda kupumzika katika kibanda.” Halafu Boazi akamwambia Ruta: “Sasa sikiliza binti yangu. Usiende kuokota masuke pahali pengine, lakini katika shamba hili tu. Ushikamane na wanawake hawa. Angalia pahali wanapovuna ufuate nyuma yao. Nimewaonya vijana hawa wasikusumbue. Na ukisikia kiu, kwenda kwenye mitungi na ukunywe maji vijana hao waliyoyateka.” Hapo Ruta akamwinamia Boazi uso mpaka chini kwa unyenyekevu, akamwambia: “Nimepata namna gani kukubaliwa mbele yako? Mbona unanishugulikia ijapokuwa mimi ni mugeni tu?” Lakini Boazi akamujibu: “Nimeyasikia yote uliyomufanyia mama mukwe wako tangu mume wako alipokufa. Ninajua jinsi ulivyowaacha wazazi wako, ukaiacha inchi yako, na jinsi ulivyokuja kuishi kati ya watu ambao haukuwajua tangu zamani. Yawe akubariki kwa yote uliyoyafanya. Yawe wa Israeli uliyemukimbilia akulinde chini ya mabawa yake, akupe zawadi kamilifu.” Ruta akamujibu: “Bwana, wewe umenifanyia wema mukubwa sana. Ingawa mimi si kama mumoja wa watumishi wako, nimetosheka kwa sababu umenifariji sana na kuongea nami kwa upendo.” Wakati wa chakula, Boazi akamukaribisha Ruta akamwambia: “Karibu hapa, kuja ukule mukate vilevile na uuchovye ndani ya divai.” Kwa hiyo Ruta akaikaa pamoja na wavunaji, na Boazi akamupa ngano iliyokaangwa, akakula akashiba hata akaacha sehemu. Naye Ruta alipoendelea kuokota mavuno, Boazi akawaambia watumishi wake: “Muache akusanye hata pahali miganda inapokuwa wala musimukaripie. Zaidi ya pale, muchomoe masuke kutoka katika miganda na mumwachie aokote bila kumukaripia.” Basi Ruta akaendelea kuokota masuke mpaka magaribi; na kisha kupepeta hiyo shayiri alipata kilo makumi tatu na zaidi. Kisha akatwaa mavuno hayo mpaka katika muji na kumwonyesha mama mukwe wake kiasi alichookota. Vilevile alikitoa kile chakula alichokiacha kisha kushiba, akamupa. Basi mama mukwe wake akamwuliza: “Uliokota wapi haya yote? Ulikuwa katika shamba la nani? Abarikiwe yule aliyekutendea wema.” Hapo Ruta akamwambia Naomi kwamba alikuwa akifanya kazi katika shamba la mutu aliyeitwa Boazi. Basi, Naomi akamwambia mukwe wake: “Yawe amubariki Boazi! Mungu anatimiza siku zote ahadi zake kwa wanaokuwa wazima na waliokufa.” Kisha akaendelea kusema: “Huyo mutu ni ndugu yetu wa karibu na ni mumoja wa wale wenye mapaswa ya kututunza.” Kisha Ruta wa Moabu akasema: “Aliniambia vilevile nishikamane pamoja na watumishi wake mpaka wamalize mavuno yote.” Basi, Naomi akamwambia Ruta: “Hakika binti yangu, ni vizuri kufanya kazi pamoja na wanawake wengine katika shamba la Boazi, kwa maana labda ungesumbuliwa kama ungekwenda katika shamba la mutu mwingine.” Kwa hiyo, Ruta akashikamana nao, akaokota masuke mpaka mavuno ya ngano na shayiri yalipomalizika. Wakati ule wote, alikuwa anakaa na mama mukwe wake. Siku moja, Naomi mama mukwe wa Ruta akamwambia: “Inanipasa kwangu kukutafutia mume kusudi upate uheri. Sasa huyu Boazi, ambaye ulifanya kazi na wajakazi wake, si ni wa ukoo wetu? Basi sikiliza, magaribi hii atakuwa katika kiwanja akipepeta shayiri. Kwa hiyo, nawa, ujipake mafuta na kuvaa vizuri, kisha uende kule katika kiwanja pahali anapopepetea. Lakini angalia usijionyeshe kwake mpaka atakapomaliza kula na kunywa. Vilevile, ujue pahali atakapolala, na akisha kusinzia, umwendee polepole uifunue miguu yake ulale pale. Yeye atakuelezea la kufanya.” Ruta akajibu: “Nitafanya yote uliyoniambia.” Kwa hiyo, Ruta akakwenda kule katika kiwanja cha kupepetea, akafanya jinsi mama mukwe wake alivyomwamuru. Boazi alipomaliza kula na kunywa, akachangamuka. Akakwenda karibu na lundo la shayiri, akalala. Ruta akakwenda polepole akafunua miguu yake na kulala pale. Katikati ya usiku, Boazi akasisimuka, akageuka, akashituka kumukuta mwanamuke amelala kwenye miguu yake. Akauliza: “Wewe ni nani?” Ruta akajibu: “Ni mimi Ruta, mujakazi wako. Kwa sababu wewe ni wa jamaa yangu wa karibu, uitande nguo yako juu ya mujakazi wako.” Boazi akasema: “Yawe akubariki, kwa maana kwa yote unayofanya unaonyesha heshima zaidi kuliko uliyoyafanya pale mbele, kwa maana haukuwatafuta vijana wamasikini au tajiri wakuoe. Sasa binti yangu usifazaike, nitakufanyia lolote utakaloomba kwa sababu kila mutu katika muji huu anajua wema wako. Ni kweli kwamba ni mapaswa yangu kukutunza, lakini kuna vilevile mwenye mapaswa ya kukutunza na ambaye ni wa karibu zaidi kuliko mimi. Kwa hiyo, kaa hapa usiku wote, na kesho asubui tutaona kama atakubali kukutunza au hapana. Ikiwa atakutunza ni vizuri. Kama vile Yawe anavyoishi, akikataa, mimi nitakutunza. Lala hapa mpaka asubui.” Basi Ruta akalala pale kwenye miguu yake mpaka asubui, lakini akaamuka asubui mapema kusudi asionekane, kwa sababu Boazi hakutaka mutu ajue kwamba Ruta alikuwa kwenye kiwanja cha kupepetea. Boazi akamwambia: “Tandika nguo yako chini.” Ruta akafanya hivyo. Boazi akamwanga shayiri yapata kilo kumi na tano, akamubebesha, naye akarudi katika muji. Alipofika katika muji, mama mukwe wake akamwuliza: “Ilikuwa namna gani binti yangu?” Ruta akamwelezea yote ambayo Boazi alimutendea. Halafu akaendelea kusema: “Akaniambia nisirudi kwa nyumba ya mama mukwe wangu mikono mitupu na kwa hiyo akanipa shayiri hii yapata kilo kumi na tano.” Naye Naomi akasema: “Sasa tulia binti yangu Ruta, mpaka uone litakalotokea. Boazi hatatulia leo mpaka ameyatimiza yote.” Boazi akakwenda kwa nafasi ya kufanyia mukutano kule kwenye mulango wa muji, akaikaa chini. Kisha yule ndugu ya Elimeleki ambaye Boazi alikuwa amemutaja, akapita karibu na pale. Boazi akamwita, akasema: “Kuja, uikae hapa ndugu.” Basi yule mutu akakuja na kuikaa pale. Halafu Boazi akawaita wazee kumi wa muji, akawaomba wao vilevile waikae pale. Wakaikaa. Halafu Boazi akamwambia yule ndugu yake: “Sasa Naomi ambaye amerudi kutoka Moabu, anataka kuuzisha shamba ambalo lilikuwa la ndugu yetu Elimeleki. Basi mimi nimeona afazali nikujulishe habari hii. Sasa ikiwa unalitaka shamba hili, ulinunue mbele ya wazee wa watu wangu. Ikiwa unalitaka au haulitaki sema basi kwa sababu nafasi ya kwanza ya kulikomboa ni yako, na yangu ni ya pili.” Naye akasema: “Mimi nitalikomboa.” Boazi akasema: “Ni vizuri, lakini ukilinunua hilo shamba kutoka kwa Naomi, ni sherti umutwae vilevile Ruta wa Moabu, mujane ambaye ni jamaa wa marehemu, kusudi shamba hilo libaki katika jamaa ya yule marehemu.” Yule ndugu aliyekuwa wa karibu akajibu: “Ikiwa ni hivyo, sitalikomboa shamba hilo, kwa sababu inaonekana kwamba nitauharibu urizi wangu. Afazali nikupe wewe haki yangu ya kulikomboa, maana mimi siwezi kulikomboa.” Siku zile katika Israeli, kama watu walitaka kukomboa au kubadilishana kitu, ilikuwa desturi kwa mutu kuonyesha kitambulisho kwa kuvua kiatu chake na kumupa mwingine. Kwa kitambulisho hicho, Waisraeli walionyesha kwamba mambo yamesawazishwa. Basi, mutu huyo alimwambia Boazi: “Ulikomboe shamba”, kisha akavua kiatu chake na kumupa. Halafu Boazi akawaambia wazee na watu waliokuwa pale: “Leo ninyi ni washuhuda wangu. Mumeona kwamba nimenunua kutoka kwa Naomi, vyote vilivyokuwa vya Elimeleki, na vya Kiliona na Malona. Zaidi ya hayo, nimemupata Ruta wa Moabu mujane wa Malona, kusudi akuwe muke wangu. Mapatano haya yatafanya mali ya jamaa ya marehemu na ukoo wake kubakia kwa watu wake katika muji huu. Ninyi ni washuhuda.” Basi wazee waliokuwa kwenye mulango na watu wote waliokuwa pale wakajibu: “Ndiyo, sisi ni washuhuda. Yawe amufanye muke wako akuwe kama Rakeli na Lea, ambao wote wawili waliijenga nyumba ya Israeli. Nawe upate kustawi katika jamaa ya Efurata, ukuwe na sifa katika Betelehemu. Yawe akupatie watoto wengi kwa njia ya mwanamuke huyu, na jamaa yako ikuwe kama ya Peresi ambaye Tamari alimuzalia Yuda.” Kwa hiyo, Boazi akamutwaa Ruta kuwa muke wake. Yawe akamujalia Ruta naye akapata mimba, akazaa mutoto mwanaume. Halafu wanawake wa muji huo wakamwambia Naomi: “Atukuzwe Yawe ambaye hakukuacha leo bila kuwa na ndugu wa kukutunza! Mujukuu wako akuwe mwenye sifa kubwa katika Israeli! Yeye atakurudishia uzima wako na atakutunza katika uzee wako. Mukwe wako ni wa lazima zaidi kwako kuliko watoto wa kiume saba, maana anakupenda na amekuzalia mujukuu huyu!” Basi Naomi akamutwaa mutoto yule akamuweka kwenye kifua chake na kuwa mulezi wake. Wanawake wajirani wakatangaza jina wakisema: “Mutoto amezaliwa kwa Naomi”, nao wakamwita jina la Obedi. Kisha Obedi akamuzaa Yese aliyemuzaa Daudi. Na hivi ndivyo vizazi vya Peresi: Peresi alimuzaa Hesironi, Hesironi akamuzaa Ramu, Ramu akamuzaa Aminadabu, Aminadabu akamuzaa Nasoni, Nasoni akamuzaa Salmoni, Salmoni akamuzaa Boazi, Boazi akamuzaa Obedi, Obedi akamuzaa Yese na Yese akamuzaa Daudi. Kulikuwa mutu mumoja katika muji wa Rama katika inchi ya milima ya Efuraimu jina lake Elekana wa kabila la Efuraimu. Yeye alikuwa mwana wa Yerohamu, na mujukuu wa Elihu mwana wa Tohu mwana wa Zufu. Elekana alikuwa na wake wawili, mumoja aliitwa Hana na wa pili Penina. Penina alikuwa na watoto, lakini Hana hakukuwa na watoto. Kila mwaka Elekana alisafiri kutoka Rama kwenda kuabudu na kumutolea Yawe wa majeshi sadaka kule Shilo. Kule, wana wawili wa Eli, Hofuni na Finehasi, walikuwa makuhani wa Yawe. Kila wakati Elekana alipotoa sadaka alimupa muke wake Penina fungu moja la nyama ya sadaka na fungu mojamoja kwa watoto wake wa kiume na wa kike. Elekana alimupa Hana fungu kubwa la nyama ya sadaka kwa sababu alimupenda sana ingawa Yawe hakumujalia watoto. Penina alikuwa akimuchokoza sana Hana kusudi amukasirikishe kwa sababu Yawe hakumujalia Hana watoto. Mambo hayo yaliendelea kila mwaka. Kila mara Hana alipokwenda kwenye nyumba ya Yawe, Penina alimukasirikisha Hana hata Hana akalia na kukataa kula chochote. Mume wake Elekana alimwuliza: “Kwa nini unalia? Kwa nini hautaki kula? Kwa nini una huzuni ndani ya moyo wako? Basi, mimi si bora kwako kuliko watoto kumi wa kiume?” Siku moja, walipokuwa wamemaliza kula na kunywa katika nyumba ya Yawe kule Shilo, Hana akasimama. Wakati ule, kuhani Eli alikuwa ameikaa kwenye kiti karibu na mulango wa nyumba ya Yawe. Hana alikuwa na huzuni sana. Na alipokuwa anamwomba Yawe akakuwa analia kwa uchungu. Akafanya kiapo akisema: “Ee Yawe wa majeshi, kama tu utayaangalia mateso yangu mimi mujakazi wako, ukinikumbuka mimi, bila kunisahau, mimi mujakazi wako, ukinijalia mimi mujakazi wako mutoto mwanaume, nitakupa wewe Yawe mutoto huyo akuwe wako maisha yake yote; wembe hautapita kwenye kichwa chake hata kidogo.” Hana aliendelea kumwomba Yawe kwa muda murefu, na kuhani Eli akakuwa anaangalia midomo yake. Hana alikuwa akiomba kimoyomoyo, midomo yake ilikuwa inachezacheza, lakini sauti yake haikusikilika. Hivyo Eli akafikiri kwamba Hana amelewa. Kwa hiyo Eli akamwambia: “Utaendelea kulewa mpaka wakati gani? Achana na kunywa divai.” Lakini Hana akamujibu: “Sivyo bwana wangu. Mimi ni mwanamuke mwenye taabu sana; mimi sijakunywa divai wala kinywaji kikali, lakini nimekuwa nikimutolea Yawe yanayokuwa ndani ya roho yangu. Usinizanie kuwa mimi ni mwanamuke asiyefaa kitu. Kwa muda wote huu nimekuwa nikisema mahangaiko yangu na taabu yangu.” Halafu Eli akamwambia: “Kwenda kwa amani; naye Mungu wa Israeli akupe kile ulichomwomba.” Hana akasema: “Ninaomba nami mujakazi wako nipate kukubaliwa mbele yako.” Hana akaenda zake, akakula chakula na hakukuwa na huzuni tena. Kesho yake asubui, Elekana na jamaa yake waliamuka asubui mapema, na kisha kumwabudu Yawe, walirudi kwao Rama. Elekana akalala na muke wake Hana na Yawe akamukumbuka. Hivyo Hana akapata mimba, akazaa mutoto wa kiume. Hana akamwita mutoto huyo Samweli, maana alisema: “Nimemwomba kwa Yawe.” Elekana na jamaa yake yote wakaenda tena Shilo na kumutolea Yawe sadaka ya kila mwaka na kutimiza kiapo. Lakini mara hii Hana hakuenda, maana alimwambia mume wake hivi: “Mara tu mutoto atakapoachishwa kunyonya, nitamupeleka kusudi awekwe mbele ya Yawe, abakie kule siku zote.” Mume wake Elekana, akamujibu: “Fanya unaloona linafaa. Ngojea mpaka utakapomwachisha mutoto kunyonya. Yawe afanye kiapo chako kuwa kweli.” Basi, Hana alibaki kwake, akaendelea kumulea mutoto wake mpaka alipomwachisha kunyonya. Alipomwachisha kunyonya alimupeleka pamoja na ngombe dume wa miaka mitatu, gunia la unga na karabia ya divai. Hana alimwingiza mutoto kwenye nyumba ya Yawe kule Shilo, naye mutoto alikuwa mudogo tu. Walipokwisha kuchinja yule ngombe dume, walimupeleka mutoto kwa kuhani Eli. Hana akamwambia: “Ee bwana wangu, kama vile unavyoishi, bwana wangu, mimi ni yule mwanamuke aliyekuwa anasimama mbele yako akimwomba Yawe. Nilimwomba anipe mutoto huyu, na yeye alinipa kile nilichomwomba. Kwa sababu hiyo, mimi ninamupa Yawe mutoto huyu; wakati wote atakapokuwa anaishi, ametolewa kwa Yawe.” Halafu, wakamwabudu Yawe pale. Halafu Hana aliomba na kusema: Ninamushangilia Yawe ndani ya moyo wangu. Ninamutukuza Yawe anayekuwa nguvu yangu. Ninawachekelea waadui zangu; maana ninaufurahia wokovu wako. Hakuna anayekuwa mutakatifu kama Yawe; hakuna yeyote anayekuwa kama yeye; hakuna anayekuwa jiwe la kufichamia kama Mungu wetu. Muache kujisifu, muache kusema kwa kiburi. Maana anayejua ni Yawe. Yeye anayapima matendo yote. Pinde za wenye nguvu, zimevunjika. Lakini wazaifu wanaendelea kupata nguvu. Wale ambao zamani walikuwa na chakula tele, sasa wanafanya kazi wapate chakula. Lakini waliokuwa na njaa, sasa hawana njaa tena. Mwanamuke tasa, amezaa watoto saba. Lakini mama mwenye watoto wengi, sasa ameachwa bila mutoto. Yawe anaua na kufufua, yeye anawashusha katika kuzimu naye anawarudisha tena. Yawe anawafanya wamoja wakuwe wamasikini, na wengine wakuwe watajiri. Anawashusha wamoja, na kuwainua wengine. Anawainua wazaifu toka katika mavumbi, anawanyanyua wakosefu toka katika majivu, na kuwaikalisha pamoja na wakubwa, na kuwarizisha viti vya heshima. Maana, minara ya dunia ni ya Yawe; yeye ameisimika dunia juu ya minara yake. Anayalinda maisha ya waaminifu wake, lakini anaangamiza maisha ya waovu katika giza. Maana, mwanadamu hapati ushindi kwa nguvu zake. Waadui za Yawe watavunjwa vipandevipande; atanguruma juu yao kama radi mbinguni. Yawe ataihukumu dunia yote, atamupa nguvu mufalme wake, na atautukuza uwezo wa muchaguliwa wake. Kisha, Elekana akarudi kwake Rama. Lakini mutoto Samweli akabaki Shilo kwa kumutumikia Yawe chini ya uongozi wa kuhani Eli. Wana wa Eli walikuwa wapotovu sana. Hawakumujali Yawe wala juu ya vitu ambavyo watu walipaswa kuwapa makuhani. Kila mara mutu alipokuwa anatolea sadaka yake, mutumishi wa kuhani alikuja na kanya yenye meno matatu; na wakati nyama ikiwa bado inatokota, huyo mutumishi alichomeka kanya ile ndani ya chungu, nyama yoyote inayonyanyuliwa na kanya ile ilikuwa mali ya kuhani. Waisraeli wote waliokwenda Shilo kutolea sadaka zao walitendewa hivyo. Zaidi ya hayo, hata mbele mafuta hayajateketezwa kwa moto, mutumishi wa kuhani anakuja na kumwambia yule mutu anayetolea sadaka: “Mumutoshee kuhani nyama ya kuchoma maana yeye hatapokea nyama yako iliyotokoteshwa, lakini inayokuwa mbichi.” Na kama mutu huyo akimujibu: “Ngojea kwanza niteketeze mafuta halafu utakamata kadiri unataka”, hapo huyo mutumishi wa kuhani anamujibu: “Hapana, unapaswa kunipatia sasa hivi. Kama sivyo, nitaitwaa kwa nguvu.” Zambi hii ya vijana hao wa Eli ilikuwa kubwa sana mbele ya Yawe. Maana, vijana hao walizarau matoleo ya Yawe. Wakati ule, kijana Samweli aliendelea kumutumikia Yawe, akiwa amevaa kizibao cha kitani. Kila mwaka mama yake alimufumia nguo ndogo, na kumupelekea alipokuwa akienda na mume wake kutolea sadaka ya kila mwaka. Eli aliwabariki Elekana na muke wake, akisema: “Yawe akupe wewe Elekana watoto wengine kwa mwanamuke huyu kusudi wakamate nafasi ya yule uliyemupa Yawe.” Kisha wao walirudi kwao. Yawe alimusikilia Hana huruma naye akajaliwa kupata watoto wa kiume watatu na wabinti wawili. Mutoto Samweli akaendelea kukomaa mbele ya Yawe. Wakati ule, Eli alikuwa muzee sana. Aliposikia yote ambayo wana wake walikuwa wanawatendea Waisraeli, jinsi walivyokuwa wanalala na wanawake waliokuwa wanatumika kwenye mulango wa Hema ya Kusanyiko, aliwauliza: “Kwa nini munafanya mambo haya? Ninasikia kutoka kwa watu wote juu ya maovu munayoyafanya. Musifanye hivyo wana wangu, kwa sababu mambo hayo ninayoyasikia kutoka kwa watu wa Yawe ni mabaya. Mutu akimukosea mwenzake, anaweza kuombewa kwa Mungu, kusudi Mungu amusamehe. Lakini mutu akimukosea Yawe nani anayeweza kumwombea musamaha?” Lakini watoto hao hawakumusikiliza baba yao, maana Yawe alikwisha kata shauri la kuwaua. Mutoto Samweli aliendelea kukomaa, akazidi kupendwa na Yawe na watu. Siku moja, mutu wa Yawe alimwendea Eli, akamwambia: “Yawe amesema hivi: Nilijijulisha kwa jamaa ya Haruni, babu yako, walipokuwa watumwa wa mufalme wa Misri katika inchi ya Misri. Kati ya makabila yote ya Israeli nilimuchagua Haruni na jamaa yake kuwa makuhani wangu, wanitumikie kwenye mazabahu, wafukize ubani na kuvaa kizibao mbele yangu. Nikaipatia jamaa ya babu yako sadaka zangu ambazo Waisraeli walinitolea kwa moto. Kwa nini basi, umezionea wivu matoleo na sadaka nilizowaamuru watu waniletee, nawe ukawaheshimu watoto wako kuliko mimi kwa kujinenepesha wenyewe kwa kula sehemu nzuri za sadaka ambazo watu wangu wa Israeli wananitolea? Kwa hiyo, ujumbe wa Yawe, Mungu wa Israeli, ni huu: Niliahidi kwamba jamaa yako na jamaa ya babu yako mutakuja mbele yangu kunitumikia milele; lakini sasa jambo hilo likuwe mbali nami. Nitawaheshimu wale wanaoniheshimu, na wale wanaonizarau, nitawazarau. –Ni ujumbe wa Yawe.– Angalia siku zinakuja ambapo nitawaua vijana wote wanaume katika jamaa yako na katika ukoo wako, hata hakutakuwa mwanaume yeyote atakayeishi na kuwa muzee. Utakuwa na wasiwasi na utawaonea wenzako wivu kwa zile baraka zote ambazo nitawapa watu wengine wa Israeli, lakini hakuna mutu katika jamaa yako atakayeishi na kuwa muzee. Mutu wako ambaye sitamwangamiza kutoka mazabahu yangu atakuwa ameponyoka kusudi nipofushe macho yake, naye atakufa moyo na wazao wake watauawa kifo kibaya. Na litakalowapata watoto wako wawili, Hofuni na Finehasi, ni hili: Wote wawili watakufa siku moja. Hiki kitakuwa ni kitambulisho kwako. Kisha, nitajiinulia kuhani mwingine mwaminifu atakayefanya kulingana na yale yanayokuwa ndani ya moyo na akili yangu. Nitamujengea ukoo imara, naye atatumika siku zote mbele ya mufalme wangu muchaguliwa. Yeyote atakayebakia katika jamaa yako atamwendea kuhani yule na kumwomba kikoroti cha feza au mukate, na kumwambia: Ninakuomba uniweke kwenye nafasi moja ya kuhani kusudi niweze kupata tu kipande cha mukate.” Wakati huo, kijana Samweli alipokuwa anamutumikia Yawe chini ya uangalizi wa Eli, ujumbe kutoka kwa Yawe ulikuwa mara haba tu; hata na maono kutoka kwake yalipatikana mara chache. Siku moja usiku, Eli ambaye macho yake yalikuwa yamefifia, alikuwa amelala katika chumba chake. Samweli naye alikuwa amelala ndani ya hekalu la Yawe karibu na Sanduku la Agano la Mungu. Taa ya Yawe ilikuwa ingali inawaka maana kulikuwa hakujapambazuka. Halafu Yawe akamwita Samweli, naye Samweli, akaitika: “Niko hapa!” Kisha Samweli akamwendea Eli kwa haraka, akamwambia: “Nimekuja, maana umeniita.” Lakini Eli akamwambia: “Mimi sikukuita. Kwenda ulale.” Samweli akarudi na kulala. Yawe akamwita tena: “Samweli!” Samweli akaamuka, akamwendea Eli na kumwambia: “Nimekuja, maana umeniita.” Lakini Eli akamwambia: “Sikukuita mwana wangu, ulale tena.” Samweli alikuwa hamujui Yawe bado, wala ujumbe wa Yawe ulikuwa bado haujafunuliwa kwake. Yawe akamwita Samweli kwa mara ya tatu. Samweli akaamuka, akamwendea Eli na kumwambia: “Nimekuja, maana umeniita.” Halafu Eli alitambua kwamba Yawe ndiye aliyemwita Samweli. Kwa hiyo Eli akamwambia Samweli: “Kwenda ulale, na akikuita, umwambie hivi: ‘Sema, ee Yawe, maana mimi mutumishi wako ninasikiliza.’ ” Hivyo Samweli akarudi na kulala pahali pake. Kisha Yawe akakuja na kusimama hapo, akamwita Samweli kama pale mbele: “Samweli! Samweli!” Samweli akasema: “Sema, maana mimi mutumishi wako ninasikiliza.” Kisha, Yawe akamwambia Samweli: “Ninataka kutenda jambo fulani katika Israeli ambalo kila mutu atakayesikia, atashituka kwa kulisikia. Siku hiyo, nitatimiza yale yote niliyosema tangu mwanzo mpaka mwisho juu ya Eli na juu ya jamaa yake. Nimekwisha kumwambia kwamba nitaiazibu jamaa yake milele, kwa uovu anaoujua kwa sababu wana wake wamenikufuru mimi na hakuwazuia. Kwa hiyo ninaapa juu ya jamaa ya Eli kwamba uovu wao hautaondolewa hata kidogo kwa matoleo wala kwa sadaka.” Samweli akalala pale mpaka asubui, kisha akaamuka na kufungua milango ya nyumba ya Yawe. Lakini Samweli aliogopa kumwambia Eli maono hayo. Hata hivyo, Eli alimwita Samweli, akamwambia: “Mwana wangu Samweli.” Samweli akaitika: “Niko hapa!” Eli akamwuliza: “Yawe alikuambia nini? Usinifiche alichokuambia. Ikiwa utanificha kitu alichokuambia, Mungu akuazibu vikali.” Basi, Samweli akamwelezea Eli yote aliyoambiwa, bila kumuficha chochote. Halafu Eli akasema: “Yeye ni Yawe; afanye anachoona ni chema kwake.” Samweli aliendelea kukomaa na Yawe akakuwa pamoja naye, na yale yote aliyosema hakuna hata moja ambalo halikutimia. Watu wote katika inchi ya Israeli toka Dani, upande wa kaskazini, mpaka Beri-Seba, upande wa kusini, wakajua kwamba Samweli alikuwa nabii mwaminifu wa Yawe. Yawe alizidi kujionyesha kule Shilo, ambako alimutokea Samweli na kuongea naye. Naye Samweli aliposema kitu, Waisraeli wote walimusikiliza. Wakati huo, Wafilistini walikutana pamoja, wapigane na Waisraeli. Waisraeli walipiga kambi yao kule Ebeni-Ezeri, na Wafilistini wakapiga kambi yao kule Afeki. Wafilistini waliwashambulia Waisraeli, na nyuma ya mapigano makali, Waisraeli walishindwa. Waisraeli elfu ine waliuawa kwenye uwanja wa vita. Waaskari walioponyoka walipofika kwenye kambi, wazee wa Israeli walisema: “Kwa nini Yawe amewaacha Wafilistini watushinde leo? Tuende tulilete Sanduku la Agano la Yawe kutoka Shilo, kusudi aweze kwenda nasi katika vita na kutuokoa kutoka waadui zetu.” Kwa hiyo, walituma watumishi kule Shilo, nao wakalileta Sanduku la Agano la Yawe wa majeshi ambaye anatawala juu ya makerubi. Wale wana wawili wa Eli, Hofuni na Finehasi walikuja pamoja na lile Sanduku la Agano la Mungu. Sanduku la Agano la Yawe lilipofika katika kambi Waisraeli wote walishangilia kwa furaha, hata inchi yote ikatikisika. Wafilistini waliposikia sauti hiyo ya furaha walisema: “Kelele hiyo yote katika kambi ya Waebrania ina maana gani?” Walipojua kwamba Sanduku la Agano la Yawe lilikuwa limefika katika kambi ya Waisraeli, Wafilistini waliogopa. Wakasema: “Bila shaka, miungu imefika katika kambi yao! Ole wetu! Jambo kama hili halijatokea tangia zamani. Ole wetu! Ni nani atakayeweza kutuokoa kutokana na miungu hiyo yenye nguvu? Hiyo ni miungu iliyowaua Wamisri kwa kila aina ya mapigo katika jangwa. Sasa, enyi Wafilistini, mujipe moyo. Mukuwe hodari kusudi musipate kuwa watumwa wa Waebrania kama wao walivyokuwa watumwa wetu. Mukuwe hodari kama wanaume na kupigana.” Wafilistini walipiga vita, na Waisraeli walishindwa na kukimbia kila mutu kwake. Siku hiyo kulikuwa mauaji makubwa maana waaskari wa miguu elfu makumi tatu wa Israeli waliuawa. Sanduku la Agano la Mungu lilitekwa, na wale wana wawili wa Eli, Hofuni na Finehasi, wakauawa. Siku hiyohiyo, mutu mumoja wa kabila la Benjamina alikimbia kutoka mustari wa mbele wa mapigano mpaka Shilo nazo nguo zake zikiwa zimechanika na akiwa na mavumbi kwenye kichwa. Eli, akiwa na wasiwasi ndani ya moyo juu ya Sanduku la Mungu, alikuwa ameikaa kwenye kiti chake, pembeni ya barabara akiangalia. Yule mutu alipofika katika muji na kueleza habari hizo, muji muzima ulilia kwa sauti. Eli aliposikia sauti ya kilio, akauliza: “Kelele hizo ni za nini?” Yule mutu akaenda haraka kwa Eli kwa kumupa habari hizo. Wakati huo, Eli alikuwa na umri wa miaka makumi kenda na nane na macho yake yalikuwa yamepofuka. Yule mutu akamwambia Eli: “Mimi nimetoka kwenye vita; nimekimbia kutoka katika vita leo.” Eli akamwuliza: “Mwana wangu, mambo yalikuwa namna gani kule?” Yule aliyeleta habari akasema: “Waisraeli wamewakimbia Wafilistini. Kumekuwa mauaji makubwa kati ya Waisraeli. Zaidi ya yote, wana wako wote wawili, Hofuni na Finehasi, wameuawa, na Sanduku la Agano la Mungu limetekwa.” Huyo mutu alipotaja tu Sanduku la Mungu, Eli alianguka machali kutoka kwenye kiti chake pembeni ya mulango. Eli alipoanguka hivyo, shingo yake ilivunjika maana alikuwa muzee na munene, naye akakufa. Eli alikuwa mwamuzi wa Israeli kwa muda wa miaka makumi ine. Tena ilitokea kwamba, mukwe wa Eli, ni kusema muke wa Finehasi, kwa wakati ule alikuwa na mimba, na muda wake wa kuzaa ulikuwa umekaribia. Aliposikia kwamba Sanduku la Agano la Mungu limetekwa na kwamba baba mukwe wake, hata na mume wake wamekufa, mara moja akapata maumivu ya kuzaa. Kwa hiyo akachutama na kuzaa. Basi, kwa sababu alikuwa karibu ya kufa, wanawake waliokuwa wanamuzalisha walimwambia: “Usiogope, maana umezaa mutoto mwanaume.” Lakini yeye hakujibu neno, wala hakuwasikiliza. Naye akamwita mutoto wake Ikabodi, maana alisema: “Utukufu wa Mungu umeondolewa kwa Waisraeli”, akiwa na maana kwamba Sanduku la Agano lilikuwa limetekwa, tena baba mukwe wake na mume wake, wote walikufa. Akasema: “Utukufu wa Mungu umeondolewa kwa Waisraeli maana Sanduku la Agano la Yawe limetekwa.” Nyuma ya Wafilistini kuliteka Sanduku la Mungu, walilibeba kutoka muji wa Ebeni-Ezeri mpaka katika muji wao wa Asidodi. Kisha, wakalipeleka Sanduku la Mungu kwenye hekalu la mungu wao Dagoni na kuliweka karibu naye. Kesho yake asubui, watu wa muji wa Asidodi walipoamuka waliona sanamu ya Dagoni imeanguka ikilalia uso chini mbele ya Sanduku la Mungu. Wakaisimamisha tena sanamu ya Dagoni na kuiweka tena pahali pake. Lakini, kesho yake asubui walipoamuka, waliona kwamba sanamu ya Dagoni imeanguka uso chini mbele ya Sanduku la Yawe, kichwa, miguu na mikono ya sanamu hiyo, vyote vilikuwa vimekatika, vikakuwa vimelala chini kwenye kizingiti cha mulango. Kiwiliwili cha sanamu ya Dagoni ndicho tu kilikuwa kimebakia. Ndiyo maana makuhani wa Dagoni na wote wanaoingia kumwabudu Dagoni kule Asidodi, wanapoingia kwenye hekalu la Dagoni hawakanyagi kizingiti cha hekalu la Dagoni mpaka leo. Yawe aliwaazibu vikali na kuwatisha watu wa Asidodi. Aliwaazibu, hata na wajirani zao, kwa kuwaletea ugonjwa wa majipu. Wakaaji wa Asidodi walipoyaona mambo yaliyowapata, wakasema: “Mungu wa Israeli anatuazibu vikali sisi pamoja na mungu wetu Dagoni. Sanduku la Agano la Yawe haliwezi kukaa kwetu.” Walituma wajumbe na kuwakusanya wakubwa wote wa Wafilistini na kuwauliza: “Tutafanya nini na Sanduku hili la Mungu wa Israeli?” Wakubwa wao wakajibu: “Sanduku hilo la Mungu wa Israeli mulipeleke Gati.” Basi, wakalipeleka kwenye muji wa Gati. Lakini kisha kulipeleka kule Gati, Yawe akauazibu muji huo, akitia hofu kubwa katika muji, na akawapiga wanaume wa muji huo, vijana kama vile wazee, kwa kuwaletea majipu. Hivyo, wakalipeleka Sanduku hilo la Mungu kwenye muji wa Ekuroni. Lakini Sanduku hilo la Mungu lilipofika kule, watu wa muji huo walipiga kelele: “Wametuletea Sanduku la Mungu wa Israeli kwa kutuua sisi na watu wetu.” Kisha wakatuma ujumbe na kukusanya wakubwa wa Wafilistini na kuwaambia: “Mulirudishe Sanduku la Mungu wa Israeli kwa nafasi yake, kusudi lisituue sisi pamoja na watu wetu.” Walifanya hivyo kwa sababu kulikuwa hofu kubwa katika muji muzima kwa sababu Mungu alikuwa anawaazibu vikali. Nao wale ambao hawakukufa walipatwa na majipu hata kilio cha muji kilifika mbinguni. Nyuma ya Sanduku la Yawe kukaa katika inchi ya Wafilistini kwa muda wa miezi saba, Wafilistini waliwaita makuhani na waaguzi wao na kuwauliza: “Tufanye nini na Sanduku hili la Yawe? Mutuambie namna gani tunavyoweza kulirudisha kwa nafasi yake.” Wao wakawaambia: “Mukirudisha Sanduku la Mungu wa Israeli, musilirudishe mikono mitupu. Lakini munapolirudisha mupeleke na sadaka ya malipo ya kosa kwa kuondoa makosa yenu. Mukifanya hivyo mutapona, nanyi mutafahamu kwa nini amekuwa akiwaazibu kwa mufululizo.” Watu wakauliza: “Tutamutolea nini kwa malipo ya makosa?” Wao wakawajibu: “Sanamu tano za zahabu mufano wa majipu, na sanamu tano za zahabu mufano wa panya, kufuatana na hesabu ya wakubwa wa Wafilistini, maana kulikuwa pigo moja tu, kwa ninyi wote na kwa wakubwa wenu. Basi mufanye sanamu zenu za majipu na sanamu za panya, vitu ambavyo vinaangamiza inchi yenu, nanyi mutamutukuza Mungu wa Israeli. Labda ataacha kuwaazibu ninyi wenyewe, miungu yenu na inchi yenu. Kwa nini munafanya mioyo yenu kuwa migumu kama Wamisri na Mufalme wao? Mungu alipowachekelea Wamisri, hawakuwaacha Waisraeli waondoke, nao wakaondoka? Basi, mutayarishe gari jipya na ngombe wawili wenye kunyonyesha ambao bado hawajafungwa nira. Muwafunge kwenye gari hilo lakini vitoto vyao visiende pamoja nao, lakini vibaki katika zizi. Mutwae Sanduku la Yawe na kuliweka katika gari hilo. Muweke zile sanamu za zahabu ambazo munamupelekea kama sadaka ya malipo ya makosa yenu pembeni ya Sanduku. Kisha muliache liende litakakokwenda. Lakini muangalie. Ikiwa gari hilo linakwenda moja kwa moja kuelekea inchi yake, ni kusema kwenye muji wa Beti-Semesi, basi, pale tutajua kwamba aliyetuletea pigo hili ni Mungu wa Israeli. Lakini kama haliendi kule, basi, tutajua kwamba sio mukono wake uliotupiga, lakini hasara hii imetupata kwa bahati mbaya.” Walifanya kama walivyoambiwa; walitwaa ngombe wawili wenye kunyonyesha na kuwafunga kwenye gari, na vitoto vyao wakavifunga katika zizi. Lile Sanduku la Yawe wakalitia kwenye gari hilo pamoja na kile kibweta chenye kuwa na sanamu za zahabu za panya na zile za majipu. Wale ngombe walikwenda moja kwa moja kuelekea muji wa Beti-Semesi bila kupinda kushoto au kuume, walikuwa wanalia walipokuwa wanakwenda. Wale wafalme watano wa Wafilistini waliwafuata mpaka kwenye mupaka wa Beti-Semesi. Watu wa Beti-Semesi walikuwa wanavuna ngano katika bonde. Walipoangalia juu na kuliona Sanduku la Yawe, wakafurahi sana. Hilo gari lilielekea kwenye shamba la Yoshua, mukaaji wa Beti-Semesi. Lilipofika hapo likasimama karibu na jiwe kubwa. Watu wakalibomoa lile gari, wakatumia mbao zake kwa kuwateketeza hao ngombe ambao waliwatoa kama sadaka ya kuteketezwa kwa Yawe. Walawi walikuwa wameliteremusha Sanduku la Yawe na kile kibweta chenye sanamu za zahabu na kuziweka kwenye lile jiwe kubwa. Basi, siku hiyo watu wa Beti-Semesi walitoa sadaka za kuteketezwa, na kumutolea Yawe sadaka. Wale wakubwa watano wa Wafilistini walipoona hayo, walirudi Ekuroni, siku ileile. Wafilistini walizipeleka zile sanamu tano za zahabu na za majipu kwa Yawe zikiwa sadaka ya malipo ya makosa yao, sanamu moja kwa ajili ya muji mumoja, muji wa Asidodi, muji wa Gaza, muji wa Asikeloni, muji wa Gati na kwa muji wa Ekuroni. Walipeleka vilevile sanamu za zahabu za panya kulingana na hesabu ya miji yote ya Wafilistini iliyotawaliwa na wakubwa watano wa Wafilistini. Miji hiyo ilikuwa yenye kuzungukwa na kuta na vijiji ambavyo havikuzungushiwa kuta. Lile jiwe kubwa kwenye shamba la Yoshua wa Beti-Semesi, pahali ambapo walilipeleka Sanduku la Yawe, ni ushuhuda wa tukio hilo mpaka leo. Yawe aliwaua wakaaji makumi saba wa muji wa Beti-Semesi, kwa sababu waliangalia ndani ya Sanduku lake. Watu waliomboleza kwa sababu Yawe alikuwa amefanya mauaji makubwa kati yao. Kisha, wakaaji wa muji wa Beti-Semesi wakasema: “Nani anayeweza kusimama mbele ya Yawe, huyu Mungu mutakatifu? Atakwenda kwa nani kusudi aondoke kwetu?” Walituma wajumbe kwenda kwa wakaaji wa muji wa Kiriati-Yearimu, waseme: “Wafilistini wamelirudisha Sanduku la Yawe, mukuje mulikamate.” Kisha, watu wa Kiriati-Yearimu wakaenda na kulikamata Sanduku la Yawe, wakalipeleka katika nyumba ya Abinadabu, aliyeishi kwenye milima. Wakamutakasa mwana wake aliyeitwa Eleazari kusudi alitunze Sanduku hilo. Tangu Sanduku la Yawe lilipopelekwa katika muji wa Kiriati-Yearimu, kulipita muda murefu, miaka makumi mbili hivi. Wakati huo Waisraeli wote walimulilia Yawe. Samweli akawaambia Waisraeli: “Kama munamurudilia Yawe kwa moyo wenu wote, basi mutupilie mbali miungu ya kigeni na sanamu za Astaroti. Muelekeze mioyo yenu kwa Yawe, na kumutumikia yeye peke yake; naye atawaokoa kutoka katika mikono ya Wafilistini.” Hivyo, Waisraeli wakatupilia mbali sanamu za Mabali na Maastaroti, wakamutumikia Yawe peke yake. Kisha, Samweli akawaita Waisraeli wote wakutane kule Misipa, akawaambia: “Kule nitamwomba Yawe kwa ajili yenu.” Hivyo, Waisraeli wote wakakusanyika kule Misipa. Walichota maji na kuyamimina mbele ya Yawe, wakafunga kula chakula siku ile yote na kusema: “Tumetenda zambi mbele ya Yawe.” Samweli akakuwa mwamuzi wa Waisraeli kule Misipa. Wafilistini waliposikia kwamba Waisraeli wamekusanyika kule Misipa, wakubwa watano wa Wafilistini wakaenda kuwashambulia. Waisraeli waliposikia juu ya jambo lile waliwaogopa Wafilistini. Basi, wakamwambia Samweli: “Usiache kumulilia Yawe, Mungu wetu, kwa ajili yetu. Endelea kumulilia atuokoe kutokana na Wafilistini.” Kwa hiyo Samweli alitwaa mwana-kondoo anayenyonya akamutolea Yawe kama sadaka ya kuteketezwa. Kisha Samweli akamulilia Yawe kwa ajili ya Waisraeli, naye akajibu kilio chake. Samweli alipokuwa anatolea ile sadaka ya kuteketezwa, Wafilistini walikaribia kuwashambulia Waisraeli. Lakini Yawe akatoa sauti kubwa ya ngurumo juu ya Wafilistini, na kuwavuruga Wafilistini, nao wakashindwa mbele ya Waisraeli. Waisraeli walitoka Misipa na kuwafuatilia Wafilistini mpaka karibu na muji wa Beti-kari, wakawaangamiza. Kisha, Samweli alitwaa jiwe na kulisimamisha kati ya Misipa na Seni, akaliita jiwe hilo “jiwe la musaada”, akisema: “Yawe ametusaidia mpaka sasa.” Siku hiyo Wafilistini walishindwa na Yawe aliwazuia Wafilistini kuishambulia inchi ya Israeli wakati wote Samweli alipokuwa anaishi. Miji yote ya Waisraeli ambayo Wafilistini waliiteka kati ya Ekuroni na Gati ilirudishiwa kwa Waisraeli. Waisraeli walikomboa inchi yao kutoka kwa Wafilistini. Tena kulikuwa amani kati ya Waisraeli na Waamori. Samweli alikuwa mwamuzi wa Israeli maisha yake yote. Kila mwaka Samweli alitembelea Beteli, Gilgali na Misipa, na kuwaamulia Waisraeli haki zao katika miji hiyo yote. Kisha, alikuwa akirudi Rama, maana kule ndiko kulikuwa kwake. Aliwaamulia Waisraeli haki zao kule, na kumujengea Yawe mazabahu kule. Samweli alipokuwa muzee, aliwafanya wana wake kuwa waamuzi wa Waisraeli. Mwana wake wa kwanza aliitwa Yoeli, na wa pili aliitwa Abiya. Wote wawili walikuwa waamuzi kule Beri-Seba. Lakini watoto hao hawakufuata mwenendo wa baba yao. Lakini walianza kujitafutia faida. Wakapokea kituliro na kupotosha haki. Basi, viongozi wote wa Waisraeli walikusanyika pamoja, na kumwendea Samweli katika muji wa Rama, wakamwambia: “Angalia, wewe sasa ni muzee na watoto wako hawafuati mwenendo wako. Hivyo, utuchagulie mufalme wa kututawala sawa vile inavyokuwa kwa mataifa mengine.” Lakini jambo la Waisraeli la kutaka wapewe mufalme wa kuwatawala, halikumupendeza Samweli. Naye akamwomba Yawe. Yawe akamwambia: “Sikiliza kila kitu ambacho watu wanakuambia; maana hawajakukataa wewe, lakini wamenikataa mimi kuwa mufalme juu yao. Tangu nilipowatoa Misri, wameniacha mimi, wamekuwa wakiitumikia miungu mingine mpaka leo. Sasa hayo matendo ambayo wamekuwa wakinitendea mimi, ndiyo wanayokutendea na wewe. Basi, uwasikilize, lakini uwaonye vikali, na uwaelezee waziwazi jinsi mufalme atakayewatawala atakavyowatendea.” Samweli akawaambia wale watu waliokuwa wanaomba wapewe mufalme maneno yote ya Yawe. Samweli aliwaambia: “Hivi ndivyo mufalme wenu atakayewatawala atakavyowatendea: wana wenu atawafanya wakuwe waendeshaji wa magari yake, na wengine kuwa waaskari wapanda-farasi wake, na wengine watapiga mbio mbele ya magari yake. Atajichagulia wengine wakuwe wakubwa wa makundi ya waaskari wake wa maelfu na wengine wakuwe wakubwa wa makundi ya watu makumi tano. Atawafanya wengine wamulimie mashamba yake na kuvuna mazao yake. Atawafanya wengine vilevile wamutengenezee silaha za vita, na wengine wamutengenezee vyombo vya magari yake. Wabinti zenu atawatwaa kuwa watengenezaji wa marasi, wengine wapishi na wengine wachomaji wa mikate. Atayatwaa mashamba yenu mazuri, mashamba ya mizeituni, na mashamba ya mizabibu na kuwapa watumishi wake. Atatwaa sehemu ya kumi ya ngano zenu na ya zabibu zenu na kuwapa wakubwa wake na watumishi wake. Atatwaa watumishi wenu na wajakazi wenu na ngombe wenu wazuri na punda wenu wazuri kabisa na kuwafanya wamufanyie kazi yake. Atatwaa sehemu ya kumi ya kondoo wenu. Na ninyi wenyewe mutakuwa watumwa wake. Wakati huo, ninyi mutalalamika kwa sababu ya mufalme wenu ambaye mumejichagulia ninyi wenyewe. Lakini Yawe hatawajibu.” Hata hivyo watu walikataa kumusikiliza Samweli, wakasema: “Hapana! Sisi tutakuwa na mufalme juu yetu, kusudi nasi vilevile tukuwe sawa mataifa mengine. Mufalme wetu, atatuamulia haki zetu, atatuongoza na kutupigania vita vyetu.” Samweli alipokwisha kusikiliza kila kitu walichosema, akaenda na kumwelezea Yawe. Yawe akamwambia Samweli: “Uwasikilize na uwapatie mufalme.” Kisha Samweli akawaambia Waisraeli warudie kwao, kila mutu katika muji wake. Katika kabila la Benjamina, kulikuwa mutu mumoja tajiri aliyeitwa Kisi. Yeye alikuwa mwana wa Abieli, mujukuu wa Zerori, wa jamaa ya Bekorati mwana wa Afia wa kabila la Benjamina. Kisi alikuwa na mwana aliyeitwa Saulo. Saulo alikuwa kijana mwenye sura nzuri, na hakuna mutu katika Israeli aliyelingana na Saulo kwa uzuri. Saulo alikuwa murefu zaidi kuliko mutu yeyote katika inchi ya Israeli; watu wote walimufikia kwenye mabega. Siku moja, punda wa Kisi, baba ya Saulo, walipotea. Hivyo, Kisi akamwambia Saulo: “Ukamate mutumishi mumoja, uende kuwatafuta punda.” Wakawatafuta kwenye inchi ya milima ya Efuraimu na eneo la Shalisa, lakini hawakuwaona kule. Halafu wakafika Salimu, na kule hawakuwaona. Wakawatafuta katika inchi ya Benjamina, hata hivyo hawakuwapata. Walipofika kwenye inchi ya Zufu, Saulo alimwambia mutumishi wake: “Turudie kwetu. Kama si vile, baba yangu ataacha kufikiri juu ya punda na kuwa na wasiwasi juu yetu.” Yule mutumishi akamwambia: “Ngoja kidogo. Katika muji huu kuna mutu wa Mungu ambaye anaheshimiwa sana. Kila neno analosema linakuwa kweli. Sasa tumwendee. Labda anaweza kutuambia jinsi safari yetu itakavyokuwa.” Saulo akamwuliza: “Lakini tukimwendea, tutamupa nini? Angalia, mikate katika mifuko yetu imekwisha na hatuna chochote cha kumupa yule mutu wa Mungu. Tuna nini?” Yule mutumishi akamujibu Saulo: “Ona, mimi nina vikoroti vine vya shekeli. Nitamupa huyo mutu wa Mungu kusudi atuambie juu ya safari yetu.” (Hapo zamani katika Israeli kama mutu akitaka kumwomba Mungu shauri, alisema: “Basi, kuja, kuja tuende kwa mwonaji.” Maana mutu anayeitwa nabii siku hizi hapo zamani aliitwa mwonaji). Saulo akamujibu: “Hilo ni jambo zuri; basi, tuende.” Hivyo, wakaenda kwenye muji mutu yule wa Mungu alimokuwa anakaa. Walipokuwa wanapanda mulima kuelekea katika muji, wakakutana na wabinti waliokuwa wakienda kuteka maji. Wakawauliza wabinti wale: “Mwonaji yuko katika muji?” Wale wabinti wakawajibu: “Ndiyo, yuko. Tena yuko mbele yenu; mukifanya haraka mutamukuta. Ameingia katika muji leo tu, kwa sababu leo watu watatoa sadaka kule kwenye mulima. Mara moja mutakapoingia katika muji, mutamukuta mbele hajakwenda kwenye nafasi ya ibada kwenye mulima kwa kula. Maana watu hawatakula mpaka kwanza yeye abariki sadaka. Kisha wale walioalikwa watakula. Hivyo muende haraka; mutakutana naye sasa hivi.” Hivyo Saulo na mutumishi wake walikwenda katika muji. Walipokuwa wanaingia katika muji, walimwona Samweli akitoka katika muji, na anaelekea kwenda kwenye nafasi ya kuabudia. Jana yake, mbele ya Saulo kufika katika muji pale, Yawe alikuwa amemwambia Samweli hivi: “Kesho, wakati kama huu, nitakuletea mutu kutoka inchi ya kabila la Benjamina, nawe utamupakaa mafuta kuwa mutawala wa watu wangu Waisraeli. Yeye atawaokoa watu wangu kutoka kwa Wafilistini, maana nimeyaona mateso ya watu wangu na kilio chao kimenifikia.” Samweli alipomwona tu Saulo, Yawe alimwambia: “Huyu ndiye mutu yule niliyekuambia. Yeye ndiye atakayewatawala watu wangu.” Hapo Saulo alimwendea Samweli aliyekuwa karibu na mulango wa muji na kumwuliza: “Ninakuomba unionyeshe nyumba ya mwonaji.” Samweli akamujibu: “Mimi ndiye mwonaji. Munitangulie kwenda kwenye nafasi ya kuabudia maana leo mutakula pamoja nami. Kesho asubui maulizo yote unayokuwa nayo nitayajibu. Na juu ya wale punda waliopotea siku tatu zilizopita, musikuwe na wasiwasi juu yao; wamekwisha kupatikana. Lakini ni nani yule ambaye Waisraeli wanamutaka sana? Si wewe na jamaa yote ya baba yako?” Saulo akajibu: “Mimi ni wa kabila la Benjamina, kabila dogo kuliko makabila yote ya Waisraeli. Na katika kabila lote la Benjamina jamaa yangu ndiyo ndogo kabisa. Lakini, kwa nini unanizungumuzia namna hiyo?” Kisha Samweli akamupeleka Saulo na mutumishi wake ndani ya baraza, akawapa nafasi ya heshima, ambako wageni walioalikwa walikuwa wameikaa. Kulikuwa wageni yapata makumi tatu. Samweli akamwambia mupishi: “Ulete ile sehemu niliyokupatia, nikakuambia uiweke pembeni.” Yule mupishi akaenda akaleta paja na sehemu ya nyama iliyokuwa upande wa juu wa paja hilo na kuviweka mbele ya Saulo. Halafu Samweli akamwambia Saulo: “Angalia kile ulichowekewa; sasa kimewekwa mbele yako. Sasa ukule kwa sababu kimewekwa kwa ajili yako kusudi upate kula pamoja na wageni.” Hivyo, Saulo akakula pamoja na Samweli siku hiyo. Waliporudi katika muji kutoka kwenye nafasi ya ibada juu ya mulima, alizungumuza na Saulo juu ya dari. Na Saulo akalala kule. Kesho yake asubui mapema, Samweli alimwita Saulo kutoka juu ya dari: “Amuka, kusudi nikusindikize urudi kwa nyumba.” Saulo aliamuka, na wote wawili, yeye na Samweli, wakatoka na kwenda katika barabara. Walipofika mwisho wa muji, Samweli akamwambia Saulo: “Umwambie yule kijana atangulie mbele yetu.” Kijana alipokwisha ondoka, Samweli akaendelea kusema: “Ngoja kidogo, nami nitakufunulia yale Mungu aliyosema.” Halafu Samweli akatwaa chupa ndogo ya mafuta akamumiminia Saulo juu ya kichwa, akamubusu na kumwambia: “Yawe amekutia mafuta ukuwe mutawala juu ya watu wake. Leo tutakapoagana, utakutana na watu wawili karibu na kaburi la Rakeli kule Zeleza katika inchi ya Benjamina. Hao watakuambia kwamba wale punda uliokuwa unawatafuta wamekwisha kupatikana. Baba yako ameacha kufikiri juu ya punda, lakini ana wasiwasi juu yako, akijiuliza kila mara: ‘Nitafanya nini juu ya mwana wangu?’ Kutoka pale utakwenda kwenye muti wa mwalo wa Tabori, pahali ambapo utakutana na wanaume watatu wakiwa katika njia kwenda kumutolea Mungu sadaka, kule Beteli. Mumoja wao atakuwa akipeleka wana-mbuzi watatu, wa pili atakuwa akipeleka mikate mitatu na wa tatu atakuwa akibeba karabia ya divai. “Watakusalimia na kukupa mikate miwili, nawe utaipokea toka katika mikono yao. Kisha, utafika kule Gibeati-Elohimu, pahali ambapo pana kambi ya waaskari wa Wafilistini. Pale, utakapokuwa unakaribia muji, utakutana na kundi la manabii. Manabii hao watakuwa wanatoka kwenye nafasi ya kuabudia na wakipiga vinubi, matari, filimbi na zeze, na watakuwa wanatabiri. Roho wa Yawe atakufikia kwa nguvu, nawe utaanza kutabiri pamoja nao na kugeuka kuwa mutu mwingine. Wakati mambo haya yatakapokutokea, chochote utakachoweza kufanya ukifanye, maana Mungu yuko pamoja nawe. Utanitangulia kwenda Gilgali, pahali ambapo nitakukuta na kutoa sadaka ya kuteketezwa na sadaka za amani. Utaningojea pale kwa muda wa siku saba mpaka nikuje na kukuonyesha la kufanya.” Saulo alipogeuka kwa kumwacha Samweli, Mungu akabadilisha moyo wa Saulo. Yale yote aliyoambiwa na Samweli yakatokea siku hiyo. Saulo na mutumishi wake walipofika kule Gibea, alipokelewa na kundi la manabii. Roho wa Mungu alimufikia kwa nguvu, na Saulo akaanza kutabiri pamoja na manabii hao. Watu waliomufahamu Saulo zamani, walipomwona anatabiri, wakaulizana: “Kitu gani kimemupata mwana wa Kisi? Hata Saulo ni mumoja wa manabii?” Mutu fulani, mukaaji wa pahali pale, akasema: “Baba yao ni nani?” Hivyo kukatokea mezali inayosema: “Hata Saulo ni mumoja wa manabii?” Saulo alipomaliza kutabiri, alikwenda kwenye nafasi ya kuabudia. Baba mudogo wa Saulo alipowaona Saulo na mutumishi, akawauliza: “Mulikuwa wapi?” Saulo akajibu: “Tulikwenda kuwatafuta punda, na tulipoona hawapatikani, tulikwenda kumwona Samweli.” Yule baba mudogo wa Saulo akamwambia: “Tafazali, uniambie kile Samweli alichokuambia.” Saulo akajibu: “Alituambia waziwazi kwamba punda wamepatikana.” Lakini Saulo hakumwelezea kwamba Samweli alimwambia kwamba atakuwa mufalme. Samweli aliwaita watu wote wakusanyike mbele ya Yawe kule Misipa. Walipofika aliwaambia: “Yawe, Mungu wa Israeli, anasema hivi: Niliwatoa Waisraeli katika inchi ya Misri, nikawaokoa ninyi kutoka kwa Wamisri na falme zingine zilizowagandamiza. Lakini leo hii mumenikataa mimi Mungu wenu ambaye ninawaokoa kutoka hasara na huzuni zenu, nanyi mumesema: ‘Hapana! Utuwekee mufalme juu yetu.’ Sasa basi, mujikusanye wote mbele yangu mukiwa katika makabila yenu na kwa maelfu yenu.” Kisha Samweli akayapanga makabila yote ya Waisraeli, kabila la Benjamina likaangukiwa na kura. Akalileta mbele kabila la Benjamina, kulingana na ukoo zake, na ukoo wa Matiri ukachaguliwa kwa kura. Mwisho akauleta mbele ukoo wa Matiri, na Saulo mwana wa Kisi akachaguliwa kwa kura. Lakini walipomutafuta hakupatikana. Wakamwuliza Mungu tena: “Kuna mutu zaidi anayekuja?” Yawe akawajibu: “Anajificha kwenye mizigo.” Basi, walikwenda mbio, wakamutafuta Saulo na kumuleta. Saulo aliposimama kati ya watu alikuwa murefu kuliko watu wote, kuanzia kwenye mabega. Samweli akawaambia watu wote: “Huyu ndiye mutu aliyechaguliwa na Yawe kati ya watu wote; hakuna yeyote anayekuwa kama yeye.” Watu wote wakapiga kelele: “Mufalme aishi milele.” Kisha, Samweli aliwaelezea watu juu ya mapaswa na haki za mufalme, akaziandika katika kitabu ambacho alikiweka mbele ya Yawe. Kisha, Samweli aliwaaga watu wote, kila mutu aende kwake. Vilevile, Saulo pamoja na wapiganaji hodari ambao zamani Mungu aligusa mioyo yao, alikwenda kwake kule katika muji wa Gibea. Lakini watu wengine wasiofaa kitu, walisema: “Mutu huyu anaweza kutuokoa?” Walimuzarau Saulo na hawakumupa zawadi yoyote. Lakini yeye hakukasirika. Mufalme Nahasi wa Waamoni, alikwenda na kuushambulia muji wa Yabesi-Gileadi. Wakaaji wa muji wa Yabesi-Gileadi wakamwambia Nahasi: “Fanya mapatano nasi, nasi tutakutumikia.” Lakini akawaambia: “Nitafanya mapatano nanyi kwa shurti hii moja: nitamwongoa kila mumoja wenu jicho lake la kuume. Hivyo nitawapatisha Waisraeli wote haya.” Wazee wa Yabesi wakamwambia: “Utupatie muda wa siku saba kusudi tuwatume wajumbe katika inchi yote ya Waisraeli. Kama hakuna mutu yeyote wa kutuokoa, tutajitoa sisi wenyewe kwako.” Wale wajumbe walipofika katika muji wa Gibea, ambako Saulo alikoishi, wakaeleza habari hizo na watu wote wakaanza kulia kwa sauti. Sasa, Saulo alikuwa anatoka kwenye shamba akiwa na ngombe dume wake, akauliza: “Watu wana nini? Kwa nini wanalia?” Wakamwambia habari wajumbe waliyoleta kutoka Yabesi. Mara moja, Saulo aliposikia maneno hayo, roho wa Mungu akamufikia kwa nguvu, naye akawaka hasira kali. Akatwaa ngombe dume wawili, akawakatakata vipande, akatuma wajumbe wapitishe vipande hivyo katika mipaka yote ya Waisraeli wakisema: “Mutu yeyote ambaye hatamufuata Saulo na Samweli katika vita, ngombe dume wake watafanyiwa hivyo.” Waisraeli waliingiwa na hofu juu ya kile ambacho Yawe angeweza kufanya. Kwa hiyo, wote walitoka pamoja. Saulo alipowapanga Waisraeli kule Bezeki akakuwa na watu elfu mia tatu kutoka inchi ya Israeli na elfu makumi tatu kutoka inchi ya Yuda. Wakawaambia wale wajumbe waliorudi kutoka Yabesi: “Muwaambie wakaaji wa Yabesi-Gileadi hivi: kesho, wakati jua linapokuwa kali, mutakuwa mumekombolewa.” Watu wa Yabesi walipopata habari hizo walifurahi sana. Hivyo, wakamuchekelea Nahasi wakimwambia: “Kesho tutajitoa wenyewe kwako, nawe utatutendea sawa unavyotaka.” Kesho yake, Saulo aliwagawanya watu katika vikundi vitatu. Wakati wa zamu ya asubui, wakaingia kwenye kambi ya adui, na kuwashambulia Waamoni. Kufikia saa sita za muchana waadui wengi walikuwa wameangamizwa. Wale waliobaki walitawanyika ovyo, hata hakukuwa kikundi chochote kati yao hata cha watu wawili tu pamoja. Halafu Waisraeli wakamwambia Samweli: “Wako wapi wale watu waliosema Saulo asikuwe mufalme juu yetu? Mutuletee watu hao, nasi tutawaua.” Lakini Saulo akawaambia: “Hakuna mutu yeyote atakayeuawa leo, kwa sababu katika siku hii, Yawe ameikomboa Israeli.” Samweli akawaambia: “Twende wote Gilgali na kwa mara ingine tutamutangaza Saulo kuwa mufalme.” Watu wote wakaenda Gilgali, na walipofika kule, wakamusimika Saulo kuwa mufalme mbele ya Yawe. Wakamutolea Yawe sadaka za amani pale. Na Saulo pamoja na watu wote wa Israeli wakafurahi sana. Samweli akawaambia Waisraeli wote: “Maneno yote muliyoniambia, nimeyasikiliza. Nimemusimika mufalme juu yenu. Sasa, munakuwa na mufalme wa kuwaongoza. Kwa upande wangu, mimi ni muzee mwenye imvi, na wana wangu wako pamoja nanyi. Nimekuwa kiongozi wenu tangu nilipokuwa kijana mpaka sasa. Niko hapa, na kama nimefanya tendo lolote baya, basi, mutoe ushuhuda mbele ya Yawe na mbele ya mufalme wake muchaguliwa. Nimenyanganya ngombe dume au punda wa mutu yeyote? Nimemugandamiza mutu yeyote? Nimemutesa mutu yeyote? Nimepokea kituliro kwa mutu yeyote kusudi nifunge macho mbele ya matendo yake? Museme nami nitamurudishia kitu chochote kile.” Watu wakamujibu: “Haujatudanganya hata kidogo, haujatugandamiza, wala haujakamata kitu chochote kwa mutu.” Samweli akajibu: “Yawe ni mushuhuda juu yenu, na mufalme wake muchaguliwa leo ni mushuhuda kuwa mumeniona sina kosa.” Wao wakajibu: “Yeye ni mushuhuda.” Samweli akawaambia: “Yawe ndiye aliyemuchagua Musa na Haruni na kuwaondoa babu zenu katika inchi ya Misri. Sasa musimame palepale munapokuwa kusudi mimi na ninyi tuhukumiwe mbele ya Yawe, nami nitawahutubia juu ya matendo yake ya ajabu ambayo aliyatenda kwa kuwaokoa ninyi na babu zenu. “Yakobo na jamaa yake walipokwenda Misri, na Wamisri walipowagandamiza, babu zenu walimulilia Yawe. Naye akawatuma Musa na Haruni ambao waliwatoa babu zenu katika inchi ya Misri na kuwafanya mukae katika inchi hii. Lakini wao walimusahau Yawe, Mungu wao, naye akawatia katika mikono ya Sisera, jemadari wa waaskari wa muji wa Hazori, na katika mikono ya Wafilistini na katika mikono ya mufalme wa Moabu. Mataifa hayo yalipigana na babu zenu na kuwashinda. Babu zenu wakamulilia Yawe, wakisema: ‘Tumefanya zambi kwa sababu tumekuacha wewe Yawe, kwa kutumikia sanamu za mungu Bali na Astaroti. Utuokoe kutoka katika mikono ya waadui zetu, nasi tutakutumikia’. Halafu Yawe alimutuma Yerubali, na kisha akamutuma Bedani, kisha Yefuta, na kwa mwisho akanituma mimi Samweli. Kila mumoja wetu aliwaokoa kutoka waadui zenu waliowazunguka, nanyi mukaishi kwa amani. Lakini mulipomwona mufalme Nahasi wa Waamoni amekuja kuwashambulia, mukamukataa Yawe ambaye ndiye Mufalme wenu, mukaniambia: ‘Hapana! Mufalme ndiye atakayetutawala’. Sasa, mufalme muliyejichagulia ndiye huyu hapa. Mulimwomba Yawe awape mufalme, naye amewapa. Kama mukimutii Yawe na kumutumikia na kusikiliza sauti yake bila kuiasi amri yake, kama ninyi wenyewe pamoja na mufalme anayewatawala mukimufuata Yawe, Mungu wenu, basi mutafanikiwa. Lakini kama hamutasikiliza sauti ya Yawe, mukiasi amri yake, basi yeye atapambana nanyi pamoja na mufalme wenu. Kwa hiyo basi, mutulie na kulitazama jambo hilo kubwa ambalo Yawe atatenda mbele yenu. Sasa si wakati wa kuvuna ngano? Lakini mimi nitamwomba Yawe alete radi na mvua, nanyi mutatambua na kuona kwamba uovu wenu muliotenda mbele ya Yawe kwa kujitakia mufalme, ni mukubwa.” Basi, Samweli akamwomba Yawe, naye akatuma radi na mvua katika siku hiyo. Watu wote wakamwogopa sana Yawe na Samweli. Hivyo wakamwambia Samweli: “Tafazali, utuombee sisi watumishi wako kwa Yawe, Mungu wako, kusudi tusikufe; kwa sababu tumezidisha zambi zetu kwa uovu huo wa kujitakia mufalme.” Samweli akawajibu: “Musiogope. Ingawa mumefanya uovu huu, musiache kumufuata Yawe, lakini mumutumikie kwa moyo wenu wote. Musiifuate miungu ya uongo isiyokuwa na faida wala haiwezi kuwaokoa, maana ni ya uongo. Kwa heshima ya jina lake kubwa, Yawe hatawatupa watu wake kwa sababu amependa kuwafanya ninyi mukuwe watu wake. Tena kwa upande wangu haitatokea niache kuwaombea kwa Yawe; kufanya hivyo itakuwa kumukosea Yawe. Nitaendelea kuwafundisha njia njema na ya haki. Basi, ninyi mumutii Yawe na kumutumikia kwa uaminifu, kwa moyo wenu wote. Mukumbuke yale mambo makubwa aliyowatendea. Lakini kama mukiendelea kutenda maovu, mutaangamia ninyi wenyewe pamoja na mufalme wenu.” Saulo alikuwa na umri wa miaka alipoanza kuwa mufalme. Na alitawala Waisraeli kwa muda wa miaka miwili.] Saulo aliwachagua Waisraeli elfu tatu. Kati yao, elfu mbili alikuwa nao kule Mikimasi na katika inchi ya milima ya Beteli. Elfu moja aliwaweka kule Gibea katika eneo la Benjamina. Hao aliwaweka chini ya uongozi wa mwana wake Yonatani. Watu wengine wote waliobakia, aliwarudisha, kila mutu kwake. Yonatani alishinda kambi ya waaskari ya Wafilistini kule Geba, na Wafilistini wote walisikia juu ya habari hiyo. Hivyo Saulo alipiga baragumu katika inchi yote, akatangaza, akisema: “Waebrania wasikie.” Waisraeli wote walisikia kwamba Saulo alikuwa ameishinda kambi ya waaskari walinzi wa Wafilistini, na kwamba Wafilistini wanawachukia sana Waisraeli. Waliitwa kwenda kuungana na Saulo kule Gilgali. Wafilistini walikuwa na magari elfu makumi tatu, waaskari elfu sita wapanda-farasi na kikundi cha waaskari wa miguu wengi kama muchanga wa bahari. Wote walipanda juu na kupiga kambi yao kule Mikimasi, upande wa mashariki wa Beti-Aweni. Waisraeli walipoona wako katika taabu (maana walikuwa wanashambuliwa vikali), walianza kujificha. Wengine walijificha katika mapango, wengine ndani ya mashimo, wengine kwenye mawe makubwa, wengine kwenye makaburi na wengine kwenye visima. Wengine walivuka muto Yordani mpaka katika inchi ya Gadi na inchi ya Gileadi. Lakini Saulo alikuwa angali kule Gilgali pamoja na watu wote waliomufuata wakitetemeka. Saulo alimungojea Samweli kwa muda wa siku saba, kama vile Samweli alivyosema. Lakini Samweli hakukuja kule Gilgali na watu walianza kumwacha Saulo. Basi, Saulo akawaambia watu: “Muniletee sadaka yenu ya kuteketezwa na zile za amani.” Naye akatolea sadaka ya kuteketezwa. Mara tu alipokuwa anamaliza kutoa sadaka ya kuteketezwa, Samweli akafika. Saulo akatoka inje kwenda kumupokea Samweli na kumusalimia. Samweli akamwuliza: “Umefanya nini?” Saulo akamujibu: “Nilipoona watu wananiacha, na wewe haukukuja katika muda wa siku ulizosema, na tena nilipoona Wafilistini wamejipanga tayari kwa vita kule Mikimasi, nikawaza kama Wafilistini watakuja kunishambulia kule Gilgali. Tena nilikuwa bado sijaomba rehema ya Yawe. Halafu nikalazimishwa kutolea mimi mwenyewe sadaka ya kuteketezwa.” Samweli akamujibu Saulo: “Umefanya kipumbafu. Haukutii mambo Yawe, Mungu wako, aliyokuamuru. Kama ungetii, Yawe angeudumisha milele ufalme wako juu ya Israeli. Lakini sasa ufalme wako hautadumu kwa sababu amri Yawe aliyokuamuru haukuitii. Yawe amejitafutia mutu mwingine ambaye atamutii kwa moyo wote, na huyo ndiye ambaye atamuchagua kuwa mutawala juu ya watu wake.” Samweli akaondoka kutoka Gilgali na kwenda kule Gibea katika inchi ya Benjamina. Saulo alipowahesabu watu waliokuwa pamoja naye, akaona wako watu mia sita tu. Saulo na mwana wake Yonatani pamoja na watu waliokuwa pamoja nao, walikaa kule Gibea katika inchi ya Benjamina na Wafilistini walipiga kambi kule Mikimasi. Wafilistini walitoka kwenye kambi yao kwenda kuwashambulia wakiwa katika vikundi vitatu. Kikundi kimoja kilielekea Ofura katika inchi ya Suali. Kikundi kingine kilielekea Beti-Horoni, na kikundi kingine kikageukia njia inayoelekea bonde la Zeboimu, kuelekea katika jangwa. Wakati huo hakukuwa mufuaji yeyote wa vyuma katika inchi nzima ya Israeli, maana Wafilistini walikusudia kuwazuia Waebrania wasipate kujitengenezea mapanga au mikuki. Kila Mwisraeli alilazimishwa kuwaendea Wafilistini kunoa majembe yake au sururu au shoka au kisu cha kuvuna. Waisraeli walikuwa wanalipa feza sehemu mbili ya tatu za shekeli kwa kunoa majembe na sururu. Na bei ya kunoa shoka au kuchongoa chuma ilikuwa sehemu moja ya tatu ya shekeli. Kwa hiyo, siku ya vita hakuna mutu kati ya wote waliokuwa pamoja na Saulo na Yonatani aliyekuwa na upanga au mukuki isipokuwa Saulo na mwana wake Yonatani. Wafilistini walipeleka kikundi cha waaskari kwenda kulinda njia ya Mikimasi. Siku moja, Yonatani mwana wa mufalme Saulo alimwambia kijana aliyemubebea silaha: “Kuja, tuende ngambo kwenye kambi ya Wafilistini.” Lakini Yonatani hakumwambia baba yake. Saulo alikuwa amepiga kambi chini ya muti wa mukomamanga kule Migroni, inje ya muji wa Gibea, akiwa pamoja na watu yapata mia sita. Ahiya mwana wa Ahitubu ndugu yake na Ikabodi mwana wa Finehasi mujukuu wa Eli kuhani wa Yawe katika muji wa Shilo, alikuwa ndiye aliyevaa kizibao cha kuhani. Watu hawakujua kwamba Yonatani amekwisha ondoka. Kwenye mapito ya mulima ambako Yonatani alipaswa kuvukia kusudi afike kwenye kambi ya Wafilistini, kulikuwa chongo mbili, upande mumoja na upande mwingine. Chongo moja iliitwa Bozezi na ingine iliitwa Sene. Chongo moja ilikuwa upande wa kaskazini wa muji wa Mikimasi na ingine ilikuwa upande wa kusini kuelekea muji wa Gibea. Yonatani akamwambia yule kijana aliyemubebea silaha: “Kuja, tuende kwenye ile kambi ya hawa watu wasiotahiriwa. Labda Yawe atatusaidia, maana Yawe haokoi kwa kutegemea wingi au uchache wa watu.” Yule kijana aliyemubebea silaha akamwambia: “Fanya chochote unachotaka kufanya, mimi niko pamoja nawe maana wazo lako ndilo wazo langu.” Yonatani akamwambia: “Tutavuka kuwaendea wale watu kusudi wapate kutuona. Kama wakituambia tuwangojee mpaka wafike hapa tunapokuwa, basi, tutasimama hapa hapa wala hatutawaendea. Lakini wakisema sisi tuwaendee, basi tutawaendea maana hicho kitakuwa ni kitambulisho kwamba Yawe amewatia katika mikono yetu.” Basi, wakajitokeza kusudi Wafilistini wawaone. Wafilistini walipowaona wakasema: “Muangalie wale Waebrania wanatoka kwenye mashimo walimokuwa wamejificha.” Wafilistini waliokuwa kwenye kambi wakamwita Yonatani na kijana aliyemubebea silaha: “Mukuje huku kwetu, nasi tutawaonyesha kitu.” Yonatani akamwambia yule kijana aliyemubebea silaha: “Unifuate. Yawe amewatia katika mikono ya Waisraeli.” Basi, Yonatani akapanda akitembea kwa miguu na mikono, na yule kijana akamufuata. Yonatani aliwashambulia Wafilistini akiwaangusha chini na yule kijana alifuata nyuma akiwaua. Katika mashambulizi hayo ya kwanza, Yonatani akiwa pamoja na kijana wake aliyemubebea silaha, aliwaua watu yapata makumi mbili katika eneo kidogo tu. Kulikuwa hofu kubwa katika kambi ya Wafilistini. Wote walianza kufazaika: waaskari katika kambi, watu katika mashamba kwenye kambi, hata na washambulizi. Inchi ilitetemeka. Hofu ilikuwa kubwa sana. Wapelelezi wa Saulo kule Gibea katika inchi ya Benjamina waliwaona watu wengi wakikimbia huku na huko. Saulo akawaambia watu waliokuwa pamoja naye: “Basi mujihesabu kwa kujua ni nani waliotutoroka.” Walipojihesabu, waligundua kwamba Yonatani na kijana aliyemubebea silaha walikuwa hawapo. Saulo akamwambia kuhani Ahiya: “Ulete hapa Sanduku la Agano la Mungu.” (Wakati huo Sanduku la Agano la Mungu lilikuwa pamoja na Waisraeli.) Saulo alipokuwa angali anaongea na kuhani, fujo katika kambi ya Wafilistini iliongezeka zaidi na zaidi. Kwa hiyo Saulo akamwambia kuhani: “Acha. Usililete tena Sanduku la Agano.” Hivyo, Saulo na watu wake wakajipanga na kuingia katika vita na Wafilistini. Lakini Wafilistini walianza kushambuliana wenyewe kwa wenyewe kwa muvurugiko mukubwa. Waebrania waliokuwa upande wa Wafilistini, na waliokwenda nao kule katika kambi, wakageuka na kujiunga na Waisraeli waliokuwa pamoja na Saulo na Yonatani. Hata Waisraeli wengine waliokuwa wamejificha kwenye inchi ya milima ya Efuraimu, waliposikia kwamba Wafilistini walikuwa wanakimbia, nao vilevile wakawafuatilia na kuwapiga. Hivyo Yawe aliwapa Waisraeli ushindi. Vita ilienea mpaka kupita Beti-Aweni. Siku ile, Waisraeli walisumbuliwa sana maana Saulo alikuwa amewaapiza watu akisema: “Alaaniwe mutu yeyote atakayekula chakula mbele jua kutua, na mbele sijajilipiza waadui zangu kisasi.” Kwa hiyo, siku yote, hakuna mutu aliyeonja chakula chochote. Watu wote walipofika katika pori, walikuta asali iliyosambaa hata chini kwenye udongo. Ingawa watu walipofika katika pori na kukuta asali ikidondoka kila nafasi, hakuna mutu aliyesubutu kula asali hiyo kwa kuogopa kile kiapo walichoapishwa. Lakini Yonatani hakusikia wakati baba yake alipowaapiza watu. Halafu akainua fimbo aliyokuwa nayo, akaichovya kwenye sega la asali, akakula asali hiyo. Hapo akajisikia kuwa na nguvu. Mutu mumoja akamwambia: “Baba yako aliwaapiza watu vikali, akisema: ‘Mutu yeyote atakayekula chakula leo alaaniwe.’ ” Nao watu walikuwa wazaifu kwa ajili ya njaa. Yonatani akajibu: “Baba yangu anawasumbua watu. Sasa mimi ninajisikia kuwa na nguvu kwa sababu nimeonja asali hii kidogo. Kama tu waaskari wetu wangeweza kula kidogo kutoka vitu walivyoteka kutoka kwa waadui zao, wengi zaidi kati ya Wafilistini wangaliuawa.” Siku ile, Waisraeli waliwapiga Wafilistini, tangu Mikimasi mpaka Ayaloni. Wakati huu Waisraeli walikuwa wamechoka kwa sababu ya njaa. Basi walikimbilia vitu walivyoteka, wakatwaa wana-kondoo, ngombe dume na wana-ngombe, wakachinja, wakakula nyama na damu. Watu wengine wakamwambia Saulo: “Angalia watu wanatenda zambi mbele ya Yawe kwa kula nyama yenye damu.” Saulo akawaambia watu: “Ninyi ni waasi. Muviringishe jiwe kubwa na kulileta hapa.” Akawaambia: “Muende muwaambie watu wote walete ngombe na kondoo wao hapa, wawachinje na kuwakula hapa. Wasitende zambi mbele ya Yawe, kwa kula nyama yenye damu.” Hivyo, usiku ule wote walipeleka ngombe wao na kuwachinjia pale. Saulo akamujengea Yawe mazabahu. Hiyo ilikuwa ndiyo mazabahu ya kwanza ambayo Saulo alimujengea Yawe. Kisha Saulo akawaambia watu: “Twende tuwafuatilie Wafilistini usiku, tuwashambulie na kunyanganya mali zao mpaka asubui. Hatutamwacha mutu yeyote muzima.” Watu wakamwambia: “Fanya unachoona kuwa chema kwako.” Lakini kuhani akawaambia: “Kwanza tuombe shauri kwa Yawe.” Hivyo, Saulo akamwuliza Mungu: “Niende kuwashambulia Wafilistini? Utawatia katika mikono ya Waisraeli?” Lakini Mungu hakujibu kitu siku hiyo. Saulo akasema: “Mukuje hapa enyi viongozi wa watu, tujue ni zambi gani tumetenda leo. Kama vile Yawe Mwokozi wa Israeli anavyoishi, hata kama ni mwana wangu Yonatani anapaswa kuuawa.” Lakini hakuna mutu aliyesema neno. Kwa hiyo, Saulo akawaambia: “Ninyi wote musimame upande ule, halafu mimi na mwana wangu Yonatani tutasimama upande huu.” Wao wakajibu: “Fanya chochote unachoona kinafaa.” Saulo akasema: “Ee Yawe wa Israeli, kwa nini haujanijibu mimi mutumishi wako? Ee Yawe wa Israeli, ikiwa kosa liko kwangu au kwa Yonatani mwana wangu, basi, jiwe la Urimu lionekane. Lakini ikiwa kosa hilo liko kwa watu wako Waisraeli, jiwe la Tumimu lionekane.” Yonatani na Saulo walipatikana kuwa na kosa, lakini watu walionekana hawana kosa. Saulo akasema: “Mupige kura kati yangu na mwana wangu Yonatani.” Yonatani akapatikana kuwa na kosa. Kwa hiyo Saulo akamwambia Yonatani: “Uniambie jambo ulilofanya.” Yonatani akajibu: “Nilikula asali kidogo kwa kutumia fimbo yangu. Niko hapa na niko tayari kufa.” Saulo akasema: “Mungu aniue ikiwa Yonatani hatauawa.” Lakini watu wakamwambia Saulo: “Kwa nini Yonatani, aliyeletea Waisraeli ushindi huu mukubwa, auawe? Haiwezikani hata kidogo. Kama vile Yawe anavyoishi, hata unywele mumoja wa kichwa chake hautaanguka chini. Alichokifanya leo, amekifanya kwa musaada wa Yawe.” Kwa hiyo, watu walimukomboa Yonatani naye hakuuawa. Kisha Saulo aliacha kuwafuatilia Wafilistini, nao Wafilistini wakarudi kwao. Saulo alipokwisha kuwa mufalme wa Waisraeli, alipigana na waadui zake wote kila upande: Wamoabu, Waamoni, Waedomu, wafalme wa Zoba na Wafilistini. Kila mara alipopigana vita, alishinda. Alipigana kwa uhodari, akawashinda Waamaleki. Aliwaokoa Waisraeli kutokana na watu wote waliowashambulia. Wana wa Saulo walikuwa: Yonatani, Iswi na Malkisua. Wabinti zake walikuwa wawili; muzaliwa wa kwanza aliitwa Merabu na mudogo aliitwa Mikali. Muke wa Saulo aliitwa Ahinoamu binti ya Ahimasi. Jemadari wa makundi ya waaskari wa Saulo aliitwa Abeneri mwana wa Neri, baba mudogo wa Saulo. Baba wa Saulo aliitwa Kisi na baba wa Abeneri aliitwa Neri mwana wa Abieli. Kulikuwa vita kali na Wafilistini kwa muda wote Saulo alipokuwa mufalme. Na kila mara Saulo alipomupata mutu mwenye nguvu au shujaa alimukamata apate kujiunga na waaskari wake. Samweli alimwambia Saulo: “Yawe alinituma kukupakaa mafuta kwa kukusimika kuwa mufalme wa watu wake Waisraeli. Sasa sikiliza maneno ya Yawe. Yawe wa majeshi anasema hivi: ‘Nitawaazibu Waamaleki kwa ajili ya mambo waliyowatendea Waisraeli: wao waliwafungia njia walipokuwa wanatoka Misri. Sasa, uende kushambulia na kuangamiza vitu vyote wanavyokuwa navyo. Usiwaache wazima, lakini uwaue wote: wanaume kwa wanawake, watoto wachanga na wenye kunyonya, ngombe, kondoo, ngamia na punda.’ ” Saulo akaita waaskari wake, akawahesabu kule Telaimu. Kulikuwa waaskari wa miguu elfu mia mbili kutoka katika inchi ya Israeli na elfu kumi kutoka inchi ya Yuda. Halafu yeye na watu wake wakaenda kwenye muji wa Amaleki, wakajificha wakivizia katika bonde. Saulo akawaambia Wakeni: “Muende! Muondoke! Mutoke kati ya Waamaleki, kama sivyo, nitawaangamiza pamoja nao. Muondoke kwa sababu ninyi muliwatendea mema Waisraeli walipotoka Misri.” Basi, Wakeni wakaondoka kati ya Waamaleki. Saulo aliwashinda Waamaleki kuanzia Havila mpaka Suri, kwa upande wa mashariki wa Misri. Alimukamata mateka mufalme Agagi wa Waamaleki akiwa angali muzima. Akawaua watu kwa makali ya upanga. Lakini Saulo na watu wake hawakumwua Agagi, kondoo bora kabisa, ngombe wazuri, wana-ngombe, wana-kondoo na chochote kile kilichokuwa kizuri hawakukiangamiza. Lakini vitu vyote vibaya na visivyokuwa vya bei kali waliviangamiza. Neno la Yawe lilimufikia Samweli kusema hivi: “Ninajuta kwamba nimemufanya Saulo kuwa mufalme. Yeye ameacha kunifuata mimi na hajatimiza amri zangu.” Samweli alikasirika, akamulilia Yawe usiku kucha. Samweli alisikia kwamba Saulo alikuwa amekwenda kule Karmeli na amesimamisha munara wa ukumbusho wake, na kwamba amekwenda Gilgali. Hivyo, kesho yake, Samweli aliamuka asubui mapema, akaenda kukutana na Saulo. Samweli alipomufikia Saulo, Saulo akamwambia Samweli: “Yawe akubariki! Nimetimiza amri ya Yawe.” Samweli akamwambia: “Mbona ninasikia mulio wa kondoo na ngombe?” Saulo akajibu: “Watu waliwaacha wazima kondoo na ngombe bora kabisa kwa kumutolea Yawe, Mungu wako, lakini wengine wote tumewaangamiza.” Samweli akamwambia Saulo: “Nyamaza! Nitakuambia jambo Yawe aliloniambia leo usiku.” Saulo akasema: “Uniambie.” Samweli akamwambia: “Ingawa unajiona kwamba wewe ni mudogo, lakini si wewe kiongozi wa makabila ya Israeli? Yawe alikupakaa mafuta kwa kukusimika kuwa mufalme juu ya Israeli. Yawe alipokutuma alikuambia: ‘Kwenda uwaangamize kabisa wale Waamaleki wenye zambi, upigane nao mpaka umewaua wote!’ Kwa nini basi, haukuitii sauti ya Yawe? Kwa nini mukakimbilia vitu kwa kuvinyanganya na hivyo kutenda jambo ovu mbele ya Yawe?” Saulo akajibu: “Nimetii sauti ya Yawe. Nilikwenda kule Yawe alikonituma; nimemuleta Agagi mufalme wa Waamaleki, na nimewaangamiza kabisa Waamaleki. Lakini watu walinyanganya vitu: kondoo, ngombe na vitu vyote bora vilivyolaaniwa kwa kumutolea Yawe, Mungu wako, kule Gilgali.” Halafu Samweli akamwambia: “Unazani kwamba Yawe anapendelea zaidi sadaka za kuteketezwa kwa moto na matoleo mengine, kuliko kuitii sauti yake? Hapana. Kumutii yeye ni bora kuliko matoleo na kumusikiliza kuliko kumutolea mafuta ya beberu. Uasi ni sawa na zambi ya kuaguza, na kiburi ni sawa na uovu wa kuabudu sanamu. Kwa sababu umeikataa amri ya Yawe, naye amekukataa kuwa mufalme.” Saulo akamwambia Samweli: “Nimetenda zambi. Nimeasi amri ya Yawe na amri yako, kwa sababu niliwaogopa watu, nikawatii wao. Lakini sasa ninakuomba, unisamehe zambi yangu. Uniruhusu nirudi pamoja nawe kusudi niweze kumwabudu Yawe.” Samweli akamujibu: “Siwezi hata kidogo kurudi pamoja nawe. Wewe umeikataa amri ya Yawe, naye amekukataa kuwa mufalme juu ya Israeli.” Samweli alipogeuka kusudi aende zake, Saulo akashika pindo la nguo yake, nayo ikapasuka. Halafu Samweli akamwambia Saulo: “Tangu leo Yawe ameurarua ufalme wa Israeli kutoka kwako na atamupa mutu mwingine kati ya wajirani zako anayekuwa bora kuliko wewe. Na Mungu ambaye ni utukufu wa Israeli hadanganyi, wala habadilishi wazo lake. Yeye si mwanadamu hata apate kubadilisha mawazo.” Saulo akajibu: “Nimefanya zambi. Hata hivyo, uniheshimishe sasa mbele ya wazee wa watu wangu na Waisraeli. Uniruhusu nirudi pamoja nawe kusudi nimwabudu Yawe, Mungu wako.” Basi, Samweli akarudi pamoja naye mpaka Gilgali na Saulo akamwabudu Yawe. Kisha Samweli akasema: “Muniletee hapa Agagi mufalme wa Waamaleki.” Agagi akamwendea Samweli akiwa mwenye furaha maana alifikiri: “Uchungu wa kifo umepita.” Samweli akasema: “Kwa sababu upanga wako umewafanya wamama wengi wasikuwe na watoto, ndivyo na mama yako atakavyokuwa bila mutoto kati ya wamama.” Akamukatakata Agagi vipandevipande mbele ya Yawe kule Gilgali. Kisha, Samweli akaenda Rama; na mufalme Saulo akarudi kwenye nyumba yake kule Gibea. Tangu siku ile, Samweli hakumwona tena Saulo, mpaka siku alipokufa. Hata hivyo Samweli alimulilia Saulo. Naye Yawe alisikitika kwamba alikuwa amemusimika Saulo kuwa mufalme juu ya inchi ya Israeli. Yawe akamwambia Samweli: “Utamulilia Saulo mpaka wakati gani? Wewe unajua kwamba mimi nimemukataa kuwa mufalme wa Israeli. Sasa, jaza ile pembe yako ya kuwekea mafuta, uondoke. Nitakutuma kwa Yese wa muji wa Betelehemu. Maana nimejipatia mufalme kati ya wana wake.” Samweli akasema: “Nitaweza kwenda namna gani? Kama Saulo akisikia habari hiyo, ataniua!” Yawe akamwambia: “Twaa mwana-ngombe pamoja nawe, na ukifika kule useme: ‘Nimekuja kumutolea Yawe sadaka’. Umwalike Yese kwenye sadaka hiyo nami nitakuonyesha la kufanya. Utamupakaa mafuta kwa ajili yangu mutu yule nitakayekutajia.” Samweli akafanya sawa alivyoambiwa na Yawe, akaenda Betelehemu. Wazee wa muji wakatoka kwenda kumupokea wakiwa wanatetemeka, wakamwuliza: “Umekuja kwa amani?” Samweli akawajibu: “Nimekuja kwa amani. Nimekuja kumutolea Yawe sadaka. Mujitakase wenyewe halafu tuende kutolea sadaka.” Samweli akamutakasa Yese pamoja na wana wake, akawakaribisha kwenye sadaka. Walipofika, naye Samweli alipomwona Eliabu, alijisemesha ndani ya moyo wake: “Hakika, muchaguliwa wa Yawe ndiye huyu anayekuwa mbele ya Yawe!” Lakini Yawe alimwambia: “Usiangalie sura yake wala urefu wake. Mimi nimemukataa maana siangalii mambo kama vile wanadamu wenye kufa wanavyoangalia. Mwanadamu anaangalia umbo la inje, lakini mimi ninaangalia ndani ya moyo.” Kisha, Yese akamwita Abinadabu na kumuleta mbele ya Samweli. Lakini Samweli akasema: “Wala huyu hakuchaguliwa na Yawe.” Yese akamuleta Shama. Samweli akasema: “Wala huyu hakuchaguliwa na Yawe.” Yese aliwapitisha wana wake wote saba mbele ya Samweli lakini Samweli akamwambia: “Yawe hajamuchagua mutu yeyote kati ya hawa.” Halafu akamwambia: “Wana wako wote wako hapa?” Yese akajibu: “Hapana, kungali mudogo wa hawa wote, lakini amekwenda kuchunga kondoo.” Samweli akamwambia: “Utume mutu amulete. Sisi hatutaikaa chini, mpaka atakapokuja hapa.” Hivyo, Yese alituma mutu, naye akaletwa. Yule kijana alikuwa mwenye afya, mwenye macho yenye kungaa na wa kupendeza. Yawe akamwambia Samweli: “Sasa, huyu ndiye; simama umupakae mafuta.” Samweli akatwaa pembe lake lenye mafuta akamupakaa Daudi mafuta mbele ya kaka zake. Mara moja roho wa Yawe akamushika Daudi kwa nguvu na kuwa naye tangu siku hiyo. Kisha Samweli akarudi katika muji wa Rama. Kisha roho wa Yawe alimwacha Saulo, na pepo muchafu kutoka kwa Yawe akamusumbua. Halafu watumishi wa Saulo wakamwambia: “Tunajua kwamba pepo muchafu kutoka kwa Mungu anakusumbua. Sasa, ee bwana wetu, amuru watumishi wako wanaokutumikia wamutafute mutu mwenye ufundi wa kupiga kinubi, na huyo pepo muchafu kutoka kwa Mungu atakapokufikia, mutu yule atapiga kinubi, nawe utapata utulivu.” Saulo akawaambia watumishi wake: “Munitafutie mutu yule anayeweza kupiga kinubi vizuri, muniletee naye.” Kijana mumoja kati ya watumishi akasema: “Nimemwona kijana mumoja wa Yese, wa muji wa Betelehemu. Kijana yule ana ujuzi wa kupiga kinubi. Yule kijana ni shujaa, hodari wa kupigana katika vita, ana hekima katika kusema na mwenye umbo zuri; Yawe yuko pamoja naye.” Hivyo, Saulo alituma ujumbe kwa Yese, na kusema: “Unitumie mwana wako Daudi, ambaye anachunga kondoo.” Yese alimutuma Daudi kwa Saulo pamoja na punda aliyebeba mikate, mufuko wa ngozi unaojaa divai na mwana-mbuzi. Daudi alipofika akaingia kwa kumutumikia Saulo. Saulo alimupenda sana, hata akamufanya akuwe mwenye kumubebea silaha zake. Halafu Saulo alituma ujumbe kwa Yese na kusema: “Umwache Daudi akae hapa anitumikie kwa sababu amepata kukubaliwa mbele yangu.” Kila mara, yule roho mwovu kutoka kwa Mungu alipomufikia Saulo, Daudi alitwaa kinubi chake na kuanza kukipiga, na roho yule alimwacha Saulo, naye akajisikia vizuri na kupata utulivu. Wafilistini walikusanya makundi yao ya waaskari kule Soko, muji unaokuwa katika inchi ya Yuda, tayari kwa vita. Walipiga kambi katika sehemu moja inayoitwa Efesi-Damimu kati ya Soko na Azeka. Saulo pamoja na Waisraeli walikusanyika, na kupiga kambi katika bonde la Ela. Wakajipanga tayari kwa kupigana na Wafilistini. Wafilistini walisimama kwenye mulima upande mumoja na Waisraeli walisimama kwenye mulima upande mwingine. Katikati yao kulikuwa bonde. Kutoka kwenye kambi ya Wafilistini, shujaa mumoja anayeitwa Goliati, wa muji wa Gati, alijitokeza. Urefu wake ulikuwa metre tatu. Kwenye kichwa chake alivaa kofia ya shaba, na nguo ya shaba kwa kifua yenye uzito wa kilo makumi tano na saba. Miguu yake vilevile ilikuwa na vikingio vya shaba na kwenye mabega yake alibeba mukuki wa shaba. Mupini wa mukuki wake ulikuwa kama muti wa mufumaji wa nguo, na chuma cha mukuki huo, kilikuwa na uzito wa kilo saba. Ngao yake ilibebwa na mutu mwingine aliyemutangulia. Goliati alisimama na kuwapigia kelele waaskari wa Waisraeli, akisema: “Munafanya nini pale? Mumekuja kupigana vita? Mimi ni Mufilistini; ninyi ni watumwa wa Saulo. Muchague mutu mumoja kati yenu akuje kupigana nami. Akinishinda na kuniua, sisi tutakuwa watumwa wenu. Lakini nikimushinda na kumwua basi, ninyi mutakuwa watumwa wetu na kututumikia.” Kisha Mufilistini yule aliendelea kusema kwa majivuno: “Ninawataka waaskari wa Waisraeli siku hii kumutoa mutu mumoja akuje kupigana nami.” Saulo pamoja na waaskari wote wa Israeli walipoyasikia maneno hayo ya Mufilistini yule, walifazaika na kuogopa sana. Daudi alikuwa mutoto wa Yese, wa ukoo wa Efurata kutoka Betelehemu katika inchi ya Yuda. Yese alikuwa na watoto wanane wa kiume. Wakati Saulo alipokuwa mufalme, yeye alikuwa amekwisha kuwa muzee, mutu mwenye umri mukubwa. Wana wakubwa watatu wa Yese, Eliabu muzaliwa wa kwanza, Abinadabu aliyefuata na Shama wa tatu, walikuwa wamekwenda pamoja na Saulo kwenye vita. Daudi alikuwa ndiye mudogo kati ya wote. Wale watoto watatu wakubwa walikuwa wamekwenda na Saulo. Ingawa Daudi mara kwa mara alikwenda kwa Saulo, alirudi kwenda Betelehemu kuchunga kondoo wa baba yake. Kwa muda wa siku makumi ine, asubui na magaribi, yule Mufilistini Goliati alijitokeza, akasimama na kuwazarau waaskari wa Waisraeli. Siku moja, Yese alimwambia mwana wake Daudi: “Uwapelekee kaka zako kilo kumi za ngano yenye kukaangwa na mikate kumi. Uwapelekee haraka kule katika kambi. Na yule mukubwa wa kundi la waaskari elfu moja umupelekee siagi hizi kumi. Uwaangalie kaka zako kama wanaendelea vizuri na kisha uniletee habari zao.” Wakati ule, mufalme Saulo, kaka za Daudi na waaskari wote wa Israeli walikuwa kwenye bonde la Ela, wanapigana na Wafilistini. Kesho yake, Daudi aliamuka asubui mapema, na akamwachia muchungaji mumoja kondoo. Alibeba chakula na kwenda kama vile alivyoagizwa na baba yake Yese. Alipofika kwenye kambi ya Waisraeli, aliwakuta wanajipanga kwenye sehemu yao ya vita na wanapiga kelele za vita. Makundi ya waaskari ya Waisraeli na ya Wafilistini walijipanga tayari kupigana vita, makundi yakiwa yanaangaliana uso kwa uso. Daudi alimupatia kile chakula mutu aliyechunga mizigo, akawakimbilia waaskari, akaenda kwa kaka zake na kuwasalimia. Alipokuwa anaongea nao, Goliati, yule shujaa wa Wafilistini kutoka Gati, alijitokeza mbele ya waaskari wa Israeli kama vile alivyozoea. Naye Daudi alimusikiliza vizuri sana. Waisraeli walipomwona Goliati, walimukimbia, na kumwogopa sana. Waliambiana: “Mumemwona yule mutu aliyejitokeza? Yeye amejitokeza kwa kuwazarau Waisraeli. Mufalme Saulo atamupa mutu yeyote atakayemwua mutu yule utajiri mwingi. Zaidi ya yote, atamupatia vilevile binti yake kusudi amwoe. Tena, watu wa jamaa ya baba yake watakuwa huru, hawatalipa kodi.” Daudi akawauliza wale waliokuwa karibu naye: “Mutu atakayemwua Mufilistini huyu na kuikomboa Israeli kutokana na haya hii atafanyiwa nini? Ni nani huyu Mufilistini, mutu mupagani, anayesubutu kuwatukana waaskari wa Mungu Mwenye Uzima?” Watu wakamwambia kama walivyokuwa wamesema pale mbele juu ya mutu atakayemwua Goliati. Lakini Eliabu, kaka mukubwa wa Daudi alipomusikia Daudi akiongea na watu, alimukasirikia Daudi, akasema: “Kwa nini umekuja? Wale kondoo wachache umemwachia nani kule katika mbuga? Ninajua majivuno yako na uovu wa moyo wako. Umekuja tu kutazama vita.” Daudi akamujibu: “Sasa nimefanya nini? Siwezi kuuliza neno tu?” Daudi akamugeukia mutu mwingine, akamwuliza neno lilelile; na kila mara alipouliza, alipata jibu lilelile. Watu fulani ambao walimusikia Daudi alivyosema, walikwenda kumwambia Saulo. Naye Saulo akaagiza aitwe. Daudi akamwambia Saulo: “Mutu yeyote asitishike ndani ya moyo wake kutokana na Mufilistini huyu. Mimi mutumishi wako nitakwenda kupigana naye.” Saulo akamwambia Daudi: “Wewe hauwezi kwenda kupigana na Mufilistini yule. Wewe ni kijana tu, lakini mutu yule amekuwa katika vita tangu ujana wake.” Daudi akasema: “Mimi mutumishi wako nimezoea kuchunga kondoo wa baba yangu. Kila wakati simba au dubu akikuja na kukamata mwana-kondoo mimi ninamufuata na kumushambulia, nikimwokoa mwana-kondoo toka katika kinywa chake. Kama simba au dubu akinishambulia, mimi ninamushika ndevu zake, nikimwangusha na kumwua. Mimi mutumishi wako nimekwisha kuua simba wengi na dubu wengi. Sasa, hata yule Mufilistini mupagani, ambaye amewatukana waaskari wa Mungu Mwenye Uzima, atakuwa kama wao. Yawe ambaye ameniokoa toka katika makucha ya simba na dubu, ataniokoa kutoka kwa Mufilistini huyu.” Saulo akamwambia: “Kwenda, naye Yawe akuwe pamoja nawe.” Saulo akamuvalisha Daudi nguo zake za kivita, akamuvalisha kofia yake ya shaba juu ya kichwa na koti lake la kifua. Daudi akajifunga upanga wa Saulo, akajaribu kutembea; lakini akashindwa kwa sababu hakuzoea nguo kama hizo. Akamwambia Saulo: “Siwezi kwenda katika vita nikiwa nimevaa nguo hizi, maana mimi sijazizoea.” Kwa hiyo, akazivua. Daudi akatwaa fimbo yake katika mukono, akajichagulia mawe matano mazuri kutoka kwenye kijito, akayatia katika mufuko wake wa muchungaji. Mujeledi wake ulikuwa tayari katika mukono wake, akaanza kumwendea Goliati Mufilistini. Yule Mufilistini, naye akaanza kumwendea Daudi, na yule aliyemubebea ngao yake akiwa mbele yake. Yule Mifilistini alipoangalia na kumwona vizuri Daudi, alimuzarau, maana Daudi alikuwa kijana muzuri mwenye afya nzuri na wa kupendeza. Goliati akamwuliza Daudi: “Sasa, hiyo fimbo ni ya nini? Unazani mimi ni imbwa hata unifikie kwa fimbo?” Mufilistini yule akamulaani Daudi kwa miungu yake. Mufilistini akamwambia Daudi: “Kuja kwangu! Mwili wako nitawapa ndege na nyama wa pori!” Lakini Daudi akamwambia Goliati: “Wewe unanifikia kwa upanga na mikuki. Lakini mimi ninakufikia kwa jina la Yawe wa majeshi, Mungu wa waaskari wa Israeli, ambaye wewe umemutukana. Siku ya leo, Yawe atakutia katika mikono yangu. Nitakushinda, nitakukata kichwa chako; na miili ya waaskari wa Wafilistini nitawapa ndege na nyama wa pori. Halafu dunia nzima itajua kwamba Mungu yuko katika Israeli. Watu wote waliokusanyika hapa leo, watajua kwamba Yawe hahitaji mikuki kwa kuwaokoa watu. Hii ni vita ya Yawe, naye atawatia ninyi wote katika mikono yetu.” Goliati akaanza tena kumwendea Daudi. Daudi akakimbia mbio kwenda kwenye mustari wa mapambano. Akatia mukono wake ndani ya mufuko wake, akatoa jiwe moja, akalirusha kwa mujeledi wake, akamupiga nalo Goliati kwenye paji la uso wake, jiwe likalipasua paji la Goliati na kupenya ndani. Goliati akaanguka uso mpaka chini. Ndivyo Daudi alivyomushinda Goliati kwa mujeledi wake na jiwe. Alimupiga yule Mufilistini na kumwua. Daudi hakukuwa na upanga wowote katika mukono wake. Basi, akaenda mbio, akasimama juu ya Goliati, akachomoa upanga wa Goliati toka katika mufuko wake, akamwua Goliati kwa kumukata kichwa chake. Wafilistini walipoona kwamba shujaa wao ameuawa, wakakimbia mbio. Halafu watu wa Israeli na watu wa Yuda walianza kupiga kelele za ushindi, wakawafuatilia Wafilistini mpaka Gati, kwenye milango ya muji wa Ekroni, hata Wafilistini walioumizwa katika vita walikufa katika njia tangu Saraimu mpaka Gati na Ekroni. Waisraeli walipotoka kuwafuatilia Wafilistini, waliteka vitu ndani ya kambi yao. Daudi alikitwaa kichwa cha yule Goliati Mufilistini, akakipeleka katika muji wa Yerusalema. Lakini silaha za Goliati akaziweka katika hema yake. Saulo alipomwona Daudi akienda kupigana na yule Mufilistini Goliati, alimwuliza Abeneri, jemadari wa kundi lake: “Abeneri, huyu ni kijana wa nani?” Abeneri alijibu: “Ee Mufalme, ninaapa kwa jina lako, mimi sijui.” Mufalme Saulo akamwambia: “Basi, uliza yeye ni kijana wa nani.” Mara tu Daudi aliporudi katika kambi nyuma ya kumwua Goliati, Abeneri alimukamata na kumupeleka kwa Saulo. Wakati ule Daudi alikuwa angali akibeba kichwa cha Goliati katika mikono yake. Saulo akamwuliza Daudi: “Kijana, wewe ni mwana wa nani?” Daudi akajibu: “Mimi ni mwana wa mutumishi wako Yese, kutoka muji wa Betelehemu.” Saulo alipomaliza kuzungumuza na Daudi, Yonatani mwana wa Saulo alivutwa sana na Daudi, akamupenda kwa moyo wake wote kama alivyojipenda yeye mwenyewe. Tangu siku ile, Saulo akamutwaa Daudi katika nyumba yake, hakumuruhusu kurudi kwenye nyumba ya baba yake. Kwa sababu Yonatani alimupenda Daudi kama roho yake, alifanya agano naye. Alivua nguo aliyovaa na kumupa Daudi pamoja na silaha zake, hata upanga, upinde na mukaba wake. Kokote Daudi alikotumwa na Saulo, Daudi alifanikiwa. Hivyo, Saulo akamufanya kuwa mukubwa wa waaskari wake. Jambo hilo liliwafurahisha watu wote hata watumishi wa Saulo. Waaskari walipokuwa wanarudi kwenye nyumba, pamoja na Daudi kisha kumwua yule Mufilistini, wanawake kutoka kila muji katika Israeli walitoka kwenda kumupokea mufalme Saulo. Wanawake nao walikuwa wanaimba nyimbo za furaha, wakipiga matari na vinubi. Vilevile walikuwa wanacheza na kuimba nyimbo za kuitikiana hivi: “Saulo ameua maelfu yake, na Daudi ameua elfu yake makumi.” Saulo hakupendezwa na maneno ya wimbo huo. Akakasirika sana. Akasema: “Wamemupa Daudi elfu makumi, lakini mimi wamenipa maelfu tu. Linalobakia ni kumupa Daudi ufalme.” Tangu siku hiyo, Saulo akakuwa anamusikilia Daudi wivu. Kesho yake, pepo muchafu kutoka kwa Mungu akamushambulia Saulo kwa rafla, akakuwa anapayukapayuka kama mwenda-wazimu katika nyumba yake. Daudi alikuwa anapiga kinubi kama alivyofanya siku zote. Saulo alikuwa na mukuki katika mukono wake. Basi, alimutupia Daudi mukuki mara mbili maana alifikiri: “Nitamubanisha Daudi kwenye ukuta.” Lakini Daudi aliepa mara zote mbili. Saulo alikuwa anamwogopa Daudi kwa sababu Yawe alikuwa pamoja naye, lakini Yawe alikuwa amemwacha Saulo. Hivyo, Saulo akamwondoa na kumufanya kiongozi wa waaskari elfu moja. Naye Daudi akawaongoza vyema katika vita. Daudi alifanikiwa katika kila kitu alichofanya, maana Yawe alikuwa pamoja naye. Saulo alipoona kufanikiwa kwa Daudi, akakuwa anamwogopa. Lakini watu wote wa Israeli na Yuda walimupenda Daudi, maana ndiye aliwaongoza vizuri katika vita na kuwarudisha na mafanikio. Saulo akamwambia Daudi: “Huyu ni Merabu, binti yangu mukubwa, nitamutoa kwako kusudi umwoe kwa masharti mawili: Ukuwe askari wangu shujaa na mutiifu, upigane vita ya Yawe.” Saulo alizani kwa njia hiyo Wafilistini watamwua Daudi, kusudi kitendo hicho asikifanye yeye mwenyewe. Daudi akamwambia Saulo: “Mimi ni nani hata mufalme akuwe baba mukwe wangu? Ukoo wangu wenyewe na hata jamaa ya baba yangu si kitu katika Israeli.” Lakini, wakati ule ambapo Merabu binti ya Saulo angeoeshwa kwa Daudi, alioeshwa kwa Adrieli kutoka muji wa Mehola. Hata hivyo, Mikali binti mwingine wa Saulo alimupenda Daudi. Saulo alipoambiwa habari ile alifurahi sana. Saulo alifikiri: “Ngoja nitamutoa Mikali kusudi akuwe mutego kwake. Na bila shaka Wafilistini watamwua.” Hivyo Saulo akamwambia Daudi kwa mara ya pili: “Sasa nitakuwa baba mukwe wako.” Halafu Saulo aliwaamuru watumishi wake akisema: “Museme na Daudi kwa siri na kumwambia: ‘Mufalme anapendezwa sana nawe, hata watumishi wake vilevile wote wanakupenda’. Hivyo, sasa ukubali kuwa mukwe wa mufalme.” Basi, watumishi hao wa Saulo walimwambia Daudi maneno hayo kwa siri, naye akawaambia: “Munazani mufalme kuwa baba mukwe wangu ni jambo dogo? Mimi ni mutu masikini na wa hali ya chini.” Wale watumishi walimwelezea Saulo kama vile Daudi alivyosema. Saulo akawaambia: “Mumwambie Daudi hivi: ‘Kile ambacho mufalme anataka kama vile mali kwa binti yake ni magovi mia moja ya Wafilistini, kusudi ajilipize kisasi kwa waadui zake.’ ” Hivi ndivyo Saulo alivyopanga kusudi Daudi auawe na Wafilistini. Wale watumishi walipomwelezea Daudi yale mapenzi ya Saulo, Daudi alifurahi kwamba mufalme atakuwa baba mukwe wake. Mbele ya siku ya arusi, Daudi na watu wake walikwenda, wakawaua Wafilistini mia mbili na kuyatwaa magovi yao mpaka kwa mufalme Saulo. Hapo akamuhesabilia hesabu kamili kusudi mufalme akuwe baba mukwe wa Daudi. Hivyo, Saulo akamupatia Daudi binti yake Mikali akuwe muke wake. Lakini Saulo alipoona wazi kwamba Yawe alikuwa pamoja na Daudi, na kwamba Mikali binti yake alimupenda sana Daudi, alizidi kumwogopa Daudi. Saulo akakuwa adui wa Daudi siku zote. Waaskari wa Wafilistini walikwenda kupigana na Waisraeli, lakini kila mara walipopigana vita, Daudi alipata ushindi kuliko watumishi wa Saulo. Hivyo jina la Daudi likazidi kusifiwa sana. Saulo alimwelezea mwana wake Yonatani na wakubwa wake juu ya mupango wake wa kumwua Daudi. Lakini Yonatani, mwana wa Saulo, alimupenda sana Daudi. Kwa hiyo, akamwambia: “Baba yangu anakusudia kukuua. Hivyo, ufanye angalisho. Kesho asubui, ujifiche pahali pa siri, ukae pale. Mimi nitakuja na kusimama karibu na baba yangu kule katika shamba pahali utakapokuwa. Pale nitaongea naye juu yako, na kitu chochote nitakachogundua kutoka kwake, nitakuelezea.” Yonatani alimusifu Daudi mbele ya baba yake, akamwambia: “Usitende zambi juu ya mutumishi wako Daudi maana yeye hajatenda zambi yoyote juu yako. Matendo yake yote siku zote yamekuwa mazuri kwako. Alipomwua yule Mufilistini Goliati, alihatarisha maisha yake, naye Yawe aliwapa Waisraeli ushindi mukubwa. Wewe ulipoona jambo lile ulifurahi. Kwa nini unataka kutenda zambi kwa kumwanga damu isiyokuwa na kosa kwa kumwua Daudi bila sababu?” Saulo alimusikiliza Yonatani, kisha akaapa: “Kama vile Yawe anavyoishi, sitamwua Daudi.” Hivyo, Yonatani akamwita Daudi na kumwelezea mambo hayo yote. Yonatani akamupeleka Daudi kwa Saulo, na Daudi akamutumikia Saulo kama hapo zamani. Kisha kulikuwa vita tena kati ya Wafilistini na Waisraeli. Daudi alitoka akapigana na Wafilistini, akawaua Wafilistini wengi na waliobaki wakamukimbia. Halafu, pepo muchafu kutoka kwa Yawe akamushika Saulo alipokuwa akiikaa ndani ya nyumba yake, akishika mukuki katika mukono, wakati Daudi alikuwa akipiga kinubi. Saulo alijaribu kumuchoma Daudi kwa mukuki ule. Lakini Daudi aliepa mukuki wa Saulo na mukuki ukapiga ukuta. Daudi akakimbia na kutoroka. Usiku ule, Saulo akatuma watu kwenye nyumba ya Daudi wamwangalie kama yuko kusudi apate kumwua asubui. Lakini Mikali muke wa Daudi akamwambia Daudi: “Kama hauopoi maisha yako usiku huu, kesho utauawa.” Kwa hiyo Mikali akamutelemusha Daudi kupitia katika dirisha, naye akatoka na kutoroka. Mikali akatwaa sanamu, akailalisha kwenye kitanda na kwenye kichwa chake akaweka kiegemeo cha manyoya ya mbuzi. Kisha akafunika kwa nguo. Saulo alipotuma watu kwa kumukamata Daudi, Mikali akawaambia kwamba Daudi ni mugonjwa. Kisha Saulo akawatuma warudie kule tena, akawaagiza akisema: “Mumulete Daudi kwangu hata akiwa katika kitanda kusudi auawe.” Wale watu walipoingia ndani ya nyumba ya Daudi na kukiangalia kitanda, waliona kuna sanamu na kiegemeo cha manyoya ya mbuzi kwenye kichwa. Halafu Saulo akamwuliza Mikali: “Kwa nini umenidanganya? Umemwacha adui yangu atoroke?” Naye Mikali akamujibu Saulo: “Aliniambia: ‘Uniache niende kusudi nisipate kukuua.’ ” Daudi alipotoroka, alikwenda Rama kwa Samweli. Alimwelezea Samweli mambo yote aliyomufanyia Saulo. Basi, Daudi na Samweli walikwenda na kukaa kule Nayoti. Kisha Saulo aliambiwa kwamba Daudi yuko kule Nayoti katika muji wa Rama. Kwa hiyo Saulo akatuma watu kwenda kumukamata. Lakini walipokuta kundi la manabii likitabiri na Samweli akiliongoza, Roho wa Mungu aliwafikia wale watumishi wa Saulo, nao vilevile wakaanza kutabiri. Saulo alipopata habari zile, alituma watumishi wengine, nao vilevile wakaanza kutabiri. Saulo akatuma watumishi wengine kwa mara ya tatu, nao vilevile wakaanza kutabiri. Kwa hiyo yeye mwenyewe akaenda Rama. Alipofika kwenye kisima kikubwa kinachokuwa kule Seku, akamukuta mutu fulani ambaye alimwuliza: “Samweli na Daudi wako wapi?” Yule mutu akamujibu: “Wako Nayoti, katika muji wa Rama.” Naye Saulo akaenda kule Nayoti katika muji wa Rama. Alipofika kule, Roho wa Mungu akamufikia, naye alianza kutabiri akiwa katika njia mpaka alipofika Nayoti katika muji wa Rama. Alivua nguo zake, akatabiri mbele ya Samweli. Alibaki uchi kwa siku moja, muchana na usiku. Kwa hiyo watu walianza kujiuliza: “Hata Saulo ni mumoja wa manabii?” Daudi alikimbia kutoka Nayoti katika Rama, akaenda mpaka kwa Yonatani, akamwambia: “Nimefanya nini? Kosa langu ni gani? Nimemutendea baba yako zambi gani hata anajaribu kuyaangamiza maisha yangu?” Yonatani akamujibu: “Jambo hilo lipite mbali nawe. Hautakufa. Baba yangu hafanyi jambo lolote, likuwe kubwa au dogo, bila kunielezea. Hata jambo hili hawezi kunificha. Sivyo inavyokuwa hata kidogo.” Daudi akaapa vilevile: “Hakika baba yako anajua vizuri kwamba nimepata kukubaliwa mbele yako. Anafikiri kukuficha juu ya jambo hili kusudi usihuzunike atakapolitenda. Lakini kweli, kama Yawe anavyoishi na kama wewe mwenyewe unavyoishi, kati yangu na lufu kuna hatua moja tu!” Yonatani akamwambia: “Neno lolote utakalosema nitakutendea nalo.” Daudi akamwambia: “Kesho ni sikukuu ya mwandamo wa mwezi, nami nilipaswa kuwa kwenye meza kwa kula pamoja na mufalme. Lakini uniache, niende kujificha kule katika shamba mpaka siku ya tatu magaribi. Baba yako akitambua kwamba siko, basi umwambie: ‘Daudi amenisihi nimupe ruhusa kusudi aende mbio katika muji wake Betelehemu, kuhuzuria kwa sadaka ya kila mwaka pamoja na jamaa yake’. Ikiwa ataona hilo ni sawa, basi, ujue kwamba mambo yangu, mimi mutumishi wako, yako sawa. Kama sivyo, kusudi lake juu yangu ni baya. Hivyo unitendee mema maana umefanya agano nami, mimi mutumishi wako, mbele ya Yawe. Lakini, kama nimefanya kosa basi, uniue wewe mwenyewe. Kwa nini unipeleke kwa baba yako kusudi aniue?” Yonatani akamujibu: “Wazo lile likuwe mbali nawe. Hakika, kama ningejua kwamba baba yangu amekusudia mabaya juu yako nisingekuficha.” Daudi akauliza: “Nitajua namna gani ikiwa baba yako atakujibu kwa ukali?” Yonatani akamujibu: “Kuja tuende ndani ya shamba!” Basi, wakaenda. Yonatani akamwambia Daudi: “Yawe, Mungu wa Israeli, akuwe mushuhuda kati yetu. Kesho au kesho kutwa, wakati kama huu nitamwuliza baba yangu. Ikiwa musimamo wake juu yako ni muzuri nitakuelezea. Yawe aniue ikiwa Saulo anakusudia kukuzuru nami nisipokujulisha kusudi uende pahali pa mbali ambapo utakuwa salama. Yawe akuwe pamoja nawe kama alivyokuwa pamoja na baba yangu. Ikiwa nitaendelea kuishi basi, unionyeshe wema wa Yawe, kusudi nisikufe, tena usiache kuitendea jamaa yangu kwa uaminifu milele. Na Yawe atakapowateketeza waadui zako kutoka katika dunia, ninaomba jina langu lisikatiliwe kabisa kutoka katika jamaa yako. Yawe awalipize kisasi waadui zako.” Kwa mara ingine tena, Yonatani alimwambia Daudi aape kulingana na upendo wake kwake yeye Yonatani, maana alimupenda Daudi kama vile anavyojipenda yeye mwenyewe. Kisha akamwambia Daudi: “Kwa sababu kesho ni sikukuu ya mwandamo wa mwezi, watu wataona wazi kwamba hauko, maana kiti chako kitakuwa wazi. Tena, kesho kutwa, watu watakukosa kabisa. Siku hiyo uende pahali ambapo ulijificha wakati jambo hili lilipokuwa lingali motomoto, ujifiche nyuma ya lundo la mawe. Mimi nitapiga mishale mitatu kandokando kama vile ninapima shabaha fulani. Nitamutuma mutumishi wangu aende kuitafuta mishale hiyo. Kama nikimwambia: ‘Angalia, mishale hiyo iko upande ule wako, uikamate’, hiyo itakuwa na maana kwamba uko salama, nawe utajitokeza kutoka pahali ulipojificha, maana, kama vile Yawe anavyoishi, kuna amani kwako, na hakuna hatari. Lakini nikimwambia ‘Angalia, mishale iko mbele yako’, kwa hiyo, ondoka. Yawe atakuwa anataka uende mbali. Kulingana na ahadi tulizowekeana, Yawe atakuwa mushuhuda kati yetu milele.” Basi, Daudi akajificha katika shamba. Wakati wa sikukuu ya mwandamo wa mwezi, mufalme Saulo akaikaa kwenye meza kwa kula. Kama ilivyokuwa kawaida yake, mufalme aliikaa kwenye kiti chake kilichokuwa karibu na ukuta. Yonatani akaikaa mbele kuelekea mufalme na Abeneri akaikaa karibu na mufalme. Lakini nafasi ya Daudi ikakuwa wazi. Siku hiyo, Saulo hakusema neno lolote, maana alifikiri kwamba labda Daudi amepatwa na tatizo au yeye si safi kwa kuhuzuria sikukuu hiyo. Siku ya pili ya sikukuu ya mwandamo wa mwezi, nafasi ya Daudi ilikuwa tu wazi. Saulo akamwuliza mwana wake Yonatani: “Kwa nini Daudi mwana wa Yese hakukuja kwenye chakula jana na leo?” Yonatani akamujibu: “Alinisihi sana nimuruhusu aende Betelehemu. Aliniambia: ‘Uniruhusu niende kwa jamaa yangu, kwa maana wanatolea sadaka kule katika muji, na ndugu yangu amenitaka nikuwe pale. Hivyo kama nimepata kukubaliwa mbele yako, uniruhusu niende kwa wandugu zangu’. Ndiyo maana hayuko hapa kushiriki chakula cha mufalme.” Kwa hiyo Saulo akawaka hasira juu ya Yonatani, akamwambia: “Mwana wa imbwa wewe! Ninajua kwamba umejichagulia mwana wa Yese kwa ajili ya haya yako mwenyewe, na kumufezehesha mama yako! Wewe, haujui kwamba wakati mwana wa Yese angali anaishi katika dunia, wewe hautaweza kuwa na uhakika wa kuwa mufalme wa inchi hii? Sasa hivi kwenda umulete hapa kwangu, kwa sababu anapaswa kuuawa.” Yonatani akamujibu: “Kwa nini auawe? Amefanya nini?” Lakini Saulo akamutupia Yonatani mikuki kusudi amwue. Naye Yonatani akatambua kwamba baba yake alikuwa amekusudia kumwua Daudi. Halafu Yonatani, akiwa amekasirika sana, aliondoka kwenye meza kwa haraka, wala hakukula chakula chochote siku hiyo ya pili ya sikukuu ya mwandamo mwezi. Yonatani alihuzunika sana juu ya Daudi kwa sababu baba yake alikuwa amemupatisha haya. Kesho yake asubui, Yonatani alikwenda kule katika shamba kwa kukutana na Daudi kama walivyoagana. Alikwenda kule na kijana mumoja wa kiume. Alipofika kule alimwambia yule kijana wake: “Kimbia uitafute mishale ambayo nitapiga.” Yule kijana alipokuwa anakimbia Yonatani akapiga mushale mbele yake. Yule kijana alipofika pahali ambapo mushale uliangukia, Yonatani akamwambia: “Mushale uko mbele yako. Fanya haraka na usisimame tu pahali pale.” Yule kijana alikusanya mishale na kumwendea bwana wake. Lakini yule kijana hakujua kitu chochote juu ya maana ya kitendo hicho. Waliojua ni Yonatani na Daudi tu. Yonatani akamupatia yule kijana silaha zake na kumwambia: “Kwenda urudi katika muji.” Yule kijana alipokwisha kuondoka, Daudi akasimama na kutoka pahali alipojificha karibu na lundo la mawe. Aliinama chini kwa heshima mara tatu mbele ya Yonatani. Wote wawili, Daudi na Yonatani, wakakumbatiana na kulia. Daudi alikuwa na uchungu zaidi kuliko Yonatani. Halafu Yonatani akamwambia Daudi: “Uende na amani. Tumekwisha wote kuapa kwa jina la Yawe kwamba Yawe akuwe mushuhuda kati yetu milele, na kati ya wazao wangu na wazao wako milele.” Daudi akasimama na kwenda zake, naye Yonatani akarudi katika muji. Daudi alikwenda kwa kuhani Ahimeleki kule Noba. Ahimeleki akaenda kumupokea akiwa anatetemeka, akamwuliza: “Kwa nini umekuja hapa peke yako?” Daudi akamujibu: “Niko hapa kutokana na amri ya mufalme. Aliniambia nisimwelezee mutu yeyote juu ya kile ambacho amenituma. Nimeagana na watu wangu kwamba tukutane pahali fulani. Uko na kitu chochote? Ninakuomba mikate mitano au chochote kinachokuwa.” Kuhani Ahimeleki akamwambia: “Hapa sina mukate wa kawaida. Niko tu na ile mikate mitakatifu. Munaweza kupewa mikate hiyo ikiwa watu wako wamejitenga na wanawake siku hizi.” Daudi akamwambia: “Kwa hakika, ninapokwenda kwa ajili ya shuguli kubwa, wanawake wanatengwa mbali nasi! Ikiwa miili ya vijana wangu inakuwa mitakatifu na safi tunapokuwa kwenye shuguli za kawaida, basi, si zaidi katika shuguli hii kubwa?” Kwa hiyo kuhani Ahimeleki akamupa mikate mitakatifu, maana hapakukuwa mikate mingine isipokuwa ile ambayo inaondolewa mbele ya Yawe na kubadilishwa na mikate mipya kutoka kwenye jiko. Basi siku ile pale kulikuwa mutumishi mumoja wa Saulo ambaye alikuwa amezuiliwa mbele ya Yawe. Mutumishi yule aliitwa Doegi Mwedomu, aliyekuwa musimamizi wa wachungaji wa nyama wa Saulo. Basi, Daudi akamwambia Ahimeleki: “Una upanga au mukuki ambao unaweza kunipatia? Kwa maana shuguli za mufalme zilinilazimisha niondoke haraka, nami niliondoka bila upanga wangu wala silaha nyingine yoyote.” Ahimeleki akamujibu: “Upanga wa Goliati Mufilistini uliyemwua kwenye bonde la Ela uko nyuma ya efodi, unafungwa katika kitambaa. Ikiwa unataka kuukamata basi, uukamate maana hakuna upanga mwingine hapa.” Daudi akamwambia: “Hakuna upanga mwingine kama huo; unipe.” Siku hiyo, Daudi alimukimbia Saulo, akaenda kwa mufalme Akisi wa Gati. Watumishi wa mufalme wakamwambia Akisi: “Huyu si Daudi, mufalme wa inchi ya Israeli? Si huyu ambaye walikuwa wakiimbiana juu yake katika ngoma, wakisema: ‘Saulo ameua maelfu yake na Daudi ameua elfu makumi yake?’ ” Daudi akafikiri sana juu ya maneno yale, akaanza kumwogopa sana Akisi mufalme wa Gati. Hivyo, akabadilisha tabia yake, akijifanya mwenda-wazimu, akakuwa anakwaruzakwaruza kwenye milango ya muji, na kuacha mate yake yatiririke kwenye ndevu zake. Akisi akawaambia watumishi wake: “Munajua kwamba mutu huyu ni mwenda-wazimu. Kwa nini mumemuleta kwangu? Ninawahitaji wenda-wazimu zaidi? Kwa nini munaniletea mwenda-wazimu akuje kunisumbua na vitendo vya wenda-wazimu? Mutu huyu ataingia katika nyumba yangu?” Daudi akaondoka kule, akakimbilia kwenye pango karibu na muji wa Adulamu. Kaka zake na wandugu zake wengine waliposikia kwamba alikuwa pale, wote walikwenda kuungana naye. Watu wote waliogandamizwa au waliokuwa na madeni au wale wenye huzuni walijiunga na Daudi. Jumla yao ilikuwa watu yapata mia ine, naye akakuwa kiongozi wao. Kutoka kule, Daudi alikwenda mpaka Misipa katika inchi ya Moabu. Akamwambia mufalme wa Moabu: “Tafazali, baba yangu na mama yangu wakae hapa kwako mpaka nijue Mungu atanifanyia nini.” Basi, Daudi aliwaacha wazazi wake wakae na mufalme wa Moabu; nao wakakaa kwake kwa muda wote ambao Daudi alikuwa katika nafasi za makimbilio. Kisha nabii Gadi akamwambia Daudi: “Usikae hapa katika makimbilio. Ondoka mara moja uende katika inchi ya Yuda.” Basi, Daudi akaondoka, akaenda katika pori la Hereti. Siku moja, Saulo alikuwa Gibea, akiikaa chini ya muti wa mukwaju, kwenye mulima, naye alikuwa na mukuki wake katika mukono na watumishi wake walikuwa wakimuzunguka. Basi akaambiwa kwamba Daudi na watu wake wameonekana. Naye Saulo akawaambia watumishi wake: “Sasa ninyi watu wa kabila la Benjamina munisikilize, munazani kwamba huyu Daudi mwana wa Yese atamupa kila mumoja wenu mashamba ya mizabibu na mashamba mengine? Au munazani kwamba atamufanya kila mumoja wenu kuwa mukubwa wa waaskari maelfu au mukubwa wa waaskari mamia? Kwa nini ninyi wote mumenifanyia shauri baya? Hakuna hata mumoja wenu anayeniambia habari hii, wakati mwana wangu anapofanya mapatano na mutoto wa Yese. Tena, kwa nini hakuna hata mumoja kati yenu anayesikitika au kunielezea kwamba mwana wangu mwenyewe anamuchochea mutumishi wangu juu yangu akinivizia kama inavyokuwa leo hii?” Kwa hiyo Doegi Mwedomu, ambaye alikuwa amesimama karibu na watumishi wa Saulo akasema: “Nilimwona mwana wa Yese alipofika Noba kwa kuhani Ahimeleki mwana wa Ahitubu. Ahimeleki alimwombea Daudi kwa Yawe, akamupa chakula na upanga wa yule Mufilistini Goliati.” Mufalme Saulo akaagiza kuhani Ahimeleki mwana wa Ahitubu pamoja na watu wote wa jamaa ya baba yake ambao walikuwa makuhani kule Noba waitwe. Wote wakamwendea mufalme Saulo. Saulo akasema: “Sasa sikiliza wewe mwana wa Ahitubu.” Ahimeleki akamujibu: “Ndiyo, bwana.” Saulo akamwambia: “Kwa nini wewe na Daudi mwana wa Yese, mumenifanyia shauri baya? Kwa nini ulimupatia mikate na upanga, halafu ukamwombea kwa Mungu? Kwa sababu hiyo, leo ameniasi na ananivizia.” Ahimeleki akamujibu: “Kati ya watumishi wako, Daudi ndiye mukubwa wa kuaminika kuliko wote. Yeye ni mukwe wako wewe mufalme mwenyewe, mukubwa wa waaskari wako walinzi na anaheshimiwa kuliko wote katika nyumba yako. Leo, sio mara ya kwanza kumwomba Mungu shauri kwa ajili yake. Mufalme, usiniwazie mimi wala mutu yeyote katika jamaa ya baba yangu juu ya mabaya yale. Mimi mutumishi wako, sijui neno lolote, likuwe kubwa au dogo juu ya jambo hilo.” Lakini mufalme Saulo akamwambia: “Ahimeleki, hakika utauawa, wewe na jamaa yote ya baba yako.” Saulo akawaambia walinzi waliokuwa wakisimama pembeni yake: “Mugeuke na kuwaua makuhani wa Yawe, maana wao wanapatana na Daudi; walijua kwamba ametukimbia wala hawakuniarifu.” Lakini walinzi hao hawakuinua mikono yao kwa kuwaua makuhani wa Yawe. Kwa hiyo, mufalme Saulo akamwambia Doegi: “Wewe geuka uwaue makuhani.” Doegi Mwedomu akaenda na kuwaua makuhani wote. Siku hiyo, Doegi aliua makuhani makumi nane na watano ambao wanavaa vizibao vya kikuhani vya kitani. Kisha aliwaua kwa makali ya upanga wakaaji wote wa Noba, muji wa makuhani, wanaume na wanawake, watoto wadogo na wenye kunyonya, ngombe, punda na kondoo. Lakini Abiatari, mumoja wa watoto wa kiume wa Ahimeleki mwana wa Ahitubu, aliponyoka akakimbilia kwa Daudi. Abiatari alimwelezea Daudi kwamba Saulo amewaua makuhani wa Yawe. Naye Daudi akamwambia Abiatari: “Nilijua wazi siku ile nilipomwona Doegi Mwedomu, kwamba atamwambia Saulo. Kwa hiyo mimi nimesababisha vifo vya watu wa jamaa ya baba yako. Wewe, ukae pamoja nami, wala usiogope. Maana, anayetafuta kuyaangamiza maisha yangu anatafuta hata yako vilevile. Ukiwa pamoja nami, uko salama kabisa.” Kisha Daudi aliambiwa: “Sikiliza, Wafilistini wanaushambulia muji wa Keila na kunyanganya ngano kwenye viwanja vya kupepetea.” Basi, Daudi akamwomba Yawe shauri: “Niende kuwashambulia Wafilistini hawa?” Yawe akamujibu: “Ndiyo, kwenda kuwashambulia Wafilistini na kuuokoa muji wa Keila.” Lakini watu wa Daudi wakamwambia: “Kama tukiwa hapahapa katikati ya inchi ya Yuda tunaogopa, itakuwa namna gani basi tukienda Keila na kushambulia waaskari wa Wafilistini?” Daudi akamwomba tena Yawe shauri, naye Yawe akamwambia: “Simama uende Keila maana nitawatia Wafilistini katika mikono yako.” Basi, Daudi akaenda Keila pamoja na watu wake, na kule akapigana na Wafilistini, akawaua Wafilistini wengi na kunyanganya ngombe wengi. Kwa hiyo Daudi aliwaokoa wakaaji wa Keila. Abiatari mwana wa Ahimeleki, alipokimbilia kwa Daudi kule Keila, alikwenda na kizibao cha kuhani. Saulo alipoambiwa kwamba Daudi amekwisha fika Keila, akasema: “Mungu amemutia katika mikono yangu maana amejifungia mwenyewe kwa kuingia katika muji wenye milango yenye vifungio.” Kwa hiyo, Saulo aliwatuma waaskari waende Keila na kufanya mashambulizi, kwa kumukamata Daudi pamoja na watu wake. Daudi aliposikia mipango miovu ya Saulo juu yake, akamwambia kuhani Abiatari: “Ulete hapa kile kizibao cha kuhani.” Kisha Daudi akaomba: “Ee Yawe, Mungu wa Israeli, kwa hakika mimi mutumishi wako, nimesikia kwamba Saulo anapanga kuja kuangamiza muji wa Keila kwa sababu yangu. Wakaaji wa Keila watanitia katika mikono ya Saulo? Saulo atakuja kweli kama nilivyosikia mimi mutumishi wako? Ee Yawe, Mungu wa Israeli, ninakuomba unijibu mimi mutumishi wako.” Yawe akamujibu: “Saulo atakuja.” Daudi akamwuliza: “Wakaaji wa Keila watanitia katika mikono ya Saulo, mimi pamoja na watu wangu?” Yawe akamujibu: “Watakutia katika mikono yake.” Kisha, Daudi na watu wake ambao walikuwa yapata mia sita, waliondoka na kwenda popote walipoweza kwenda. Saulo aliposikia kwamba Daudi amekwisha kimbia kutoka Keila, akaiacha mipango yake yote. Basi, Daudi alibaki katika makimbilio ndani ya jangwa, katika inchi ya milima ya mbuga za Zifu. Saulo alimutafuta kila siku, lakini Mungu hakumutia Daudi katika mikono yake. Daudi alijua kwamba Saulo alitaka kuyaangamiza maisha yake. Daudi akabaki katika mbuga za Zifu, kule Horeshi. Yonatani mwana wa Saulo akamufuata Daudi kule Horeshi, akamutia moyo kwamba Mungu anamulinda. Yonatani akamwambia: “Usiogope, baba yangu Saulo hatakupata. Wewe utakuwa mufalme wa Israeli, mimi nitakuwa wa pili wako. Hata Saulo baba yangu anajua jambo hili.” Hao wote wawili, wakafanya agano mbele ya Yawe. Daudi akabaki katika muji wa Horeshi na Yonatani akaenda zake kwenye nyumba. Saulo alipokuwa angali kule Gibea, Wazifu wakamwendea na kumwambia: “Daudi anajificha katika inchi yetu kwenye makimbilio kule Horeshi, kwenye mulima Hakila, unaokuwa upande wa kusini wa jangwa. Sasa, mufalme, ukuje kusudi utimize mambo yanayokuwa ndani ya moyo wako, na kwa upande wetu, kazi yetu itakuwa kumutia Daudi katika mikono yako.” Saulo akawajibu: “Ninyi kweli munanionea huruma; Yawe awabariki. Muende tena muhakikishe, mujue pahali anapojificha, na ni nani amemwona pahali pale; maana nimeambiwa kwamba yeye ni mwerevu sana. Muchunguze kila upande mujue pahali anapojificha, kisha muniletee habari kamili. Halafu nitakwenda pamoja nanyi na ikiwa angali kule, basi, mimi nitamutafuta kati ya maelfu yote ya watu wa Yuda.” Basi, wakaondoka kwenda Zifu, wakimutangulia Saulo. Wakati ule, Daudi na watu wake walikuwa katika mbuga za Maoni, katika bonde la Araba upande wa kusini wa jangwa. Saulo na watu wake wakaanza kumutafuta Daudi. Lakini Daudi alipopata habari zile, alikwenda kujificha kwenye mawe makubwa, yanayokuwa katika mbuga za Maoni na kukaa kule. Saulo aliposikia habari zile, alimufuatilia Daudi kule kwenye mbuga za Maoni. Saulo na watu wake walikuwa upande mumoja wa mulima, na Daudi na watu wake walikuwa upande mwingine wa mulima. Daudi alipokuwa anaharakisha kukimbia, Saulo naye alikuwa anamukaribia kwa kumukamata Daudi. Hapo mutu mumoja akamwendea Saulo na kumwambia: “Kuja haraka; Wafilistini wanaishambulia inchi.” Kwa hiyo, Saulo akaacha kumufuatilia Daudi, akaenda kupigana na Wafilistini. Ndiyo maana pahali pale pakaitwa “Jiwe la Matengano.” Daudi aliondoka pahali pale, akaenda kuishi kwenye makimbilio ya muji wa Engedi. Saulo aliporudi kutoka kupigana na Wafilistini, alipata habari kwamba Daudi yuko kwenye mbuga za Engedi. Kisha Saulo aliwatwaa waaskari elfu tatu waliochaguliwa waliokuwa bora zaidi katika inchi yote ya Israeli, akaenda kumutafuta Daudi na watu wake pahali panapoitwa “Mawe ya Mbuzi wa Pori.” Saulo alipokuwa anasafiri, alifika kwenye pango moja lililokuwa karibu na zizi la kondoo, akaingia mule ndani ya pango kwa kujisaidia. Daudi na watu wake walikuwa wakiikaa ndani kabisa ya pango lile. Watu wa Daudi wakamwambia: “Ile siku Yawe aliyokuambia kwamba atakuja kumutia adui yako katika mikono yako nawe umutendee utakavyoona inafaa, leo imefika.” Halafu Daudi alimwendea Saulo polepole kutoka nyuma, akakata pindo la nguo yake. Daudi akaanza kufazaika ndani ya moyo kwa sababu alikata pindo la nguo ya Saulo kwa siri. Akawaambia watu wake: “Yawe anizuie nisimutendee kitendo kama hiki bwana wangu ambaye ni muchaguliwa wa Yawe. Nisiunyooshe mukono wangu juu ya mutu ambaye Yawe amemupakaa mafuta.” Kwa maneno hayo, Daudi akawashawishi watu wake wasimuzuru Saulo; aliwakataza wasimushambulie. Kisha Saulo akasimama, akatoka ndani ya pango akaendelea na safari yake. Kisha, Daudi naye akasimama, akatoka ndani ya pango na kumwita Saulo: “Bwana wangu mufalme!” Mufalme Saulo alipoangalia nyuma, Daudi aliinama mpaka chini, kwa kumuheshimu Saulo. Kisha akamwambia: “Kwa nini unawasikiliza watu wanaokuambia: ‘Daudi anataka kukuzuru’? Sasa, leo umejionea kwa macho yako mwenyewe. Ulipokuwa ndani ya pango Yawe alikutia katika mikono yangu. Wamoja kati ya watu wangu waliniambia nikuue, lakini nilikuhurumia. Nikasema sitanyoosha mukono wangu juu ya bwana wangu maana yeye ni muchaguliwa wa Yawe. Angalia, baba yangu, angalia pindo hili la nguo yako katika mikono yangu. Kwa kulikata pindo la nguo yako bila kukuua, unaweza sasa kujua kwa hakika kwamba mimi si mwovu wala mwasi. Mimi sijatenda zambi juu yako ingawa wewe unaniwinda uniue. Yawe aamue kati yangu na wewe. Naye ndiye akulipize kisasi lakini mimi sitanyoosha mukono wangu juu yako hata kidogo. Kumbuka mezali ya kale inayosema ‘Uovu unatoka ndani ya mwovu’, lakini sitanyoosha mukono juu yako. Sasa wewe mufalme wa Israeli angalia mutu unayetaka kumwua! Unamufuatilia nani? Unafuatilia imbwa yenye kufa! Unakifuatilia kiroboto! Basi, Yawe akuwe mwamuzi kati yangu na wewe. Yeye aliangalie jambo hili, anitetee na kuniokoa katika mikono yako.” Daudi alipomaliza kusema, Saulo akasema: “Hiyo ni sauti yako mwana wangu Daudi?” Saulo akalia kwa sauti. Kisha akamwambia Daudi: “Wewe una haki kuliko mimi; umenilipa mazuri, wakati mimi nimekulipa mabaya. Leo, umeonyesha jinsi unavyokuwa muzuri kwangu. Haukuniua ijapokuwa Yawe alinitia katika mikono yako. Mutu akimukamata adui yake atamwacha aende salama? Kwa lile ulilonitendea, Yawe akupe zawadi njema! Sasa nimejua kwamba hakika utakuwa mufalme wa Israeli, na ufalme wa Israeli utaimarishwa chini yako. Lakini uniapie kwa jina la Yawe kwamba hautawateketeza wazao wangu, wala kufuta kabisa jina langu katika jamaa ya baba yangu.” Daudi akamwapia Saulo. Kisha Saulo akarudia kwake, lakini Daudi na watu wake wakaenda kwenye nafasi zao za makimbilio. Sasa, Samweli akakufa. Nao Waisraeli wote wakakusanyika kwa kumwomboleza. Wakamuzika kwenye nyumba yake kule Rama. Kisha Daudi akaenda zake kwenye jangwa za Parani. Kulikuwa mutu mumoja kule katika muji wa Maoni ambaye alikuwa na biashara ya kondoo katika muji wa Karmeli. Kule Karmeli alifuga kondoo wake na kuwakata manyoya. Alikuwa tajiri sana. Alikuwa na kondoo elfu tatu na mbuzi elfu moja. Mutu yule aliitwa Nabali na muke wake aliitwa Abigaili. Abigaili alikuwa mwanamuke mwenye akili na sura nzuri. Lakini Nabali alikuwa mutu wa chuki na mutenda maovu; tena alikuwa wa ukoo wa Kalebu. Basi, Daudi akiwa kule katika jangwa alisikia kwamba Nabali alikuwa anawakata kondoo wake manyoya kule Karmeli. Kwa hiyo, akawatuma vijana kumi, akawaambia: “Mwende kwa Nabali kule Karmeli mumupelekee salamu zangu. Mutamwambia kwamba Daudi anakusalimia hivi: ‘Amani ikuwe kwako, kwa jamaa yako na yote unayokuwa nayo. Nimesikia kwamba unawakata kondoo wako manyoya. Ninataka ujue kwamba wachungaji wako walikuwa pamoja nasi, nasi hatukuwazuru. Tena muda wote walipokuwa pamoja nasi katika muji wa Karmeli, hawakukosa kitu chochote. Ukiwauliza, watakuambia. Sasa ninakuomba vijana wangu hawa wapate kukubaliwa mbele yako, maana tumefika wakati wa sikukuu. Tafazali uwapatie kitu chochote unachokuwa nacho watumishi wako hawa nami mwana wako Daudi.’ ” Wale vijana wa Daudi walikwenda na kumwambia Nabali kama walivyoagizwa na Daudi. Halafu wakangojea kidogo. Kisha Nabali akawajibu watumishi wa Daudi: “Daudi ni nani? Mwana wa Yese ni nani? Siku hizi kuna watumishi wengi wanaowakimbia wabwana zao. Nikamate mikate yangu, maji yangu na nyama niliyowachinjia wakata manyoya ya kondoo wangu na kuwapa watu ambao sijui hata wanatoka wapi?” Basi, wale vijana wa Daudi walirudi na kumwambia Daudi namna walivyojibiwa. Kwa hiyo Daudi akawaambia watu wake: “Kila mutu apakatie upanga wake kwenye kiuno.” Kila mutu akapakatia upanga wake, na Daudi vilevile akapakatia upanga wake. Watu yapata mia ine wakamufuata Daudi na watu mia mbili wakabaki na mizigo. Kijana mumoja wa Nabali, akamwambia Abigaili, muke wa Nabali: “Daudi alituma wajumbe toka katika jangwa kuja kumusalimia bwana wetu. Lakini yeye aliwatukana. Lakini watu hao walikuwa wema sana kwetu, hawakutuzuru; na wakati wote tulipokuwa nao kule katika jangwa hatukukosa kitu chochote. Kwetu, walikuwa kama ukuta wa ulinzi usiku na muchana muda wote tulipokuwa tunawachunga kondoo. Sasa ufikiri juu ya jambo hili na uamue la kufanya. Jambo hili linaweza kuleta hasara kwa bwana wetu na jamaa yake yote. Yeye ni mutu mubaya na hakuna anayeweza kusema naye.” Abigaili akafanya haraka, akatwaa mikate mia mbili, mifuko miwili ya ngozi ya mbuzi yenye kujaa divai, kondoo watano waliotayarishwa vizuri, kilo kumi na saba za ngano zenye kukaangwa, vishada mia moja vya zabibu zenye kukauka, mikate ya tini mia mbili, na vitu hivi vyote akavipakia juu ya punda. Akamwambia yule kijana wake: “Utangulie! Mimi nitakufuata.” Lakini hakumwambia mume wake neno lolote. Alipokuwa anateremuka, akipanda juu ya punda wake, na kukingwa na mulima upande mumoja, akakutana kwa rafla na Daudi na watu wake wakiwa wanaelekea upande anakotoka. Daudi alikuwa akifikiri: “Mimi nimekuwa nikilinda mali yote ya Nabali katika jangwa bila faida yoyote na hakuna kitu chake chochote kilichopotea, naye amenilipa mabaya kwa mazuri niliyomutendea. Mungu aniue mimi ikiwa kesho asubui nitakuwa sijawaua wanaume wake wote.” Abigaili alipomwona tu Daudi, akashuka mara moja kutoka juu ya punda wake, na kuinama mbele ya Daudi mpaka uso wake ukagusa chini. Alijitupa kwenye miguu ya Daudi na kumwambia: “Bwana wangu, kosa lote likuwe juu yangu tu. Ninakuomba niongee nawe mimi mujakazi wako. Ninakuomba usikilize maneno ya mujakazi wako. Usimwangalie Nabali ambaye ni mutu mubaya. Maana jina lake la Nabali linamustahili. Yeye anaitwa Nabali; na kweli yeye ni mutu mupumbafu. Bwana wangu, wale vijana wako ulipowatuma, mimi mujakazi wako sikuwaona. Sasa bwana wangu, kama vile Yawe anavyoishi na kama vile unavyoishi, unaona kwamba Yawe amekuzuia kulipiza kisasi kwa kumwanga damu na hivyo upate kuwa na kosa. Uwaache waadui zako na wale wote wanaokutakia mabaya wakuwe wapumbafu kama Nabali. Bwana wangu, ninakuomba upokee zawadi hii niliyokuletea, na uwape vijana wanaokufuata. Ninakuomba unisamehe mimi mujakazi wako. Yawe atakupa jamaa imara kwa sababu, wewe bwana wangu, unapigana vita ya Yawe. Wakati wote wa maisha yako usipatikane na ubaya wowote. Kukitokea watu wanaokufuatilia na kutaka kuyaangamiza maisha yako, Yawe, Mungu wako, atayalinda maisha yako pamoja na watu wanaokuwa wazima. Lakini atayatupilia mbali maisha ya waadui zako, kama vile mutu anavyotupa jiwe kwa mujeledi. Nyuma ya Yawe kukutendea mazuri yote aliyokuahidi, na kukuchagua kuwa mutawala wa Israeli, wewe bwana wangu, hautakuwa na sababu ya kujuta wala kuhukumiwa na zamiri kutokana na kumwanga damu bila sababu kwa kujilipiza kisasi. Lakini, Yawe atakapokuwa amekutendea vizuri, ninakuomba, bwana wangu, unikumbuke mimi mujakazi wako.” Daudi akamwambia Abigaili: “Atukuzwe Yawe, Mungu wa Israeli, aliyekutuma leo kukutana nami. Umutukuze Yawe aliyekupa hekima kwa kunizuia kuwa na kosa la umwangaji wa damu na kujilipiza kisasi mimi mwenyewe. Kwa hakika, kama Yawe, Mungu wa Israeli, anavyoishi, amenizuia kukuzuru. Usingefanya haraka kuja kukutana nami, kwa hakika, kesho asubui hakuna mwanaume yeyote wa Nabali ambaye angebaki.” Kisha, Daudi akapokea vitu vyote ambavyo Abigaili alikuwa amemuletea, akamwambia Abigaili: “Rudi kwako na amani. Mimi nimeyasikia uliyosema, na ombi lako nimelipokea.” Abigaili aliporudi kwake, alimukuta Nabali akifanya karamu kubwa katika nyumba yake kama ya kifalme. Nabali alikuwa akifurahi sana ndani ya moyo maana alikuwa amelewa sana. Kwa hiyo hakumwambia neno lolote mpaka asubui. Asubui, Abigaili alipoona kwamba divai imemutoka mume wake, alimwelezea mambo yote, na palepale Nabali akapooza, akakuwa kama jiwe. Kisha siku kumi, Yawe alimupiga Nabali akakufa. Daudi aliposikia kwamba Nabali amekufa, alisema: “Atukuzwe Yawe ambaye amemulipiza kisasi Nabali kwa kunitukana, naye Yawe ameniepusha mimi mutumishi wake kutenda maovu. Yawe amemwazibu Nabali kwa uovu wake.” Kisha Daudi alituma watu kwa kumuchumbilia Abigaili akuwe muke wake. Watumishi wa Daudi walipofika kwa Abigaili kule Karmeli, wakamwambia: “Daudi ametutuma kukutwaa kusudi ukuwe muke wake.” Abigaili alisimama, na kuinama mbele yao uso mpaka chini, akasema: “Mimi ni mujakazi tu. Niko tayari kunawisha miguu ya watumishi wa bwana wangu.” Abigaili alifanya haraka, akasimama na kupanda juu ya punda wake, akifuatana na wajakazi wake watano, akaenda na watumishi wa Daudi. Akakuwa muke wake. Tena Daudi alimwoa Ahinoamu wa Yezereheli. Hivyo hao wawili wakakuwa wake zake. Wakati huo, Saulo alikuwa amemwoesha binti yake Mikali, ambaye alikuwa muke wa Daudi, kwa Palti mwana wa Laisi, wa muji wa Galimu. Wamoja kati ya wanaume kutoka muji wa Zifu wakamwendea Saulo kule Gibea, wakamwambia kwamba Daudi alikuwa anajificha kwenye mulima Hakila, upande wa mashariki wa Yesimoni. Mara moja, Saulo alikwenda kwenye jangwa la Zifu kumutafuta Daudi akiwa na waaskari waliochaguliwa elfu tatu wa Israeli. Saulo akapiga kambi juu ya mulima Hakila, karibu na barabara, upande wa mashariki wa Yesimoni. Lakini Daudi alikuwa angali kule katika jangwa. Daudi alipojua kwamba Saulo alikuwa amekuja katika jangwa kwa kumutafuta, alituma wapelelezi, akafahamishwa kwamba ni kweli. Daudi akatoka, akaenda pahali Saulo alipopiga kambi. Akaona pahali ambapo Saulo alikuwa amelala. Saulo alikuwa pamoja na Abeneri mwana wa Neri, mukubwa wa waaskari, katikati ya kambi akizungukwa na waaskari wake. Daudi akamwambia Ahimeleki ambaye alikuwa Muhiti, na Abisai ndugu ya Yoabu (mama yao aliitwa Zeruya): “Nani atakwenda pamoja nami kwenye kambi ya Saulo?” Abisai akamwambia: “Mimi nitakwenda pamoja nawe.” Kwa hiyo usiku, Daudi na Abisai wakaingia kwenye kambi ya Saulo, wakamukuta Saulo amelala katikati ya kambi hiyo, na mukuki wake umechomekwa katika udongo karibu na kichwa chake. Abeneri pamoja na waaskari walikuwa wamelala na kumuzunguka Saulo. Abisai akamwambia Daudi: “Leo Mungu amemutia adui yako katika mikono yako. Basi, uniache nimushindilie katika udongo kwa pigo moja tu la mukuki. Sitamupiga mara mbili.” Lakini Daudi akamwambia Abisai: “Usimwangamize; maana nani anaweza kunyoosha mukono wake juu ya mutu ambaye ni muchaguliwa wa Yawe, naye asiazibiwe? Kama vile Yawe anavyoishi, Yawe mwenyewe atamwua, au siku yake ya kufa itamufikia au atakuja kwenda katika vita na kuangamizwa kule. Lakini Yawe anakataza nisinyooshe mukono wangu juu ya mutu ambaye ni muchaguliwa wa Yawe. Lakini twaa mukuki wake unaokuwa karibu na kichwa chake pamoja na mufuko wake wenye maji, halafu tujiendee zetu.” Kwa hiyo, Daudi alitwaa ule mukuki na mufuko wa maji karibu na kichwa cha Saulo nao wakajiendea zao. Lakini hakuna mutu aliyeona au kujua tukio hilo, wala hakuna aliyeamuka, maana Yawe aliwaletea usingizi muzito. Kisha, Daudi akaenda upande wa pili wa bonde hilo, akasimama juu kwenye mulima mbali na kundi la Saulo. Akawaita kwa sauti waaskari wa Saulo na Abeneri mwana wa Neri akisema: “Abeneri, unanisikia?” Abeneri akauliza: “Wewe ni nani unayemwita mufalme?” Daudi akamujibu: “Wewe si mwanaume? Nani anayekuwa sawa nawe katika Israeli? Mbona basi, haukumulinda bwana wako mufalme? Mutu mumoja kati yetu aliingia pale kwa kumwangamiza bwana wako mufalme! Ulilotenda si jambo zuri. Kama vile Yawe anavyoishi, unastahili kufa, maana haukumulinda bwana wako, ambaye ni muchaguliwa wa Yawe. Sasa angalia, mukuki wa mufalme na ule mufuko wa maji uliokuwa karibu na kichwa chake kama vipo!” Saulo alitambua sauti ya Daudi, akamwuliza: “Hiyo ni sauti yako mwana wangu Daudi?” Daudi akamujibu: “Bwana wangu mufalme, ni sauti yangu.” Halafu akaendelea kusema: “Lakini kwa nini, wewe bwana wangu unanifuatilia mimi mutumishi wako? Nimefanya nini? Ni uovu gani nimekufanyia? Basi, sasa bwana wangu mufalme, usikie maneno ya mutumishi wako. Ikiwa Yawe ndiye aliyekuchochea ukuje kunishambulia, basi, apokee sadaka ambayo itamusukuma kubadilisha mawazo yake. Lakini ikiwa ni watu, basi, Yawe awalaani watu hao maana wamenifukuza kutoka urizi ambao Yawe aliotupa wakisema: ‘Kwenda uitumikie miungu mingine.’ Usiniache nikufe katika inchi ya kigeni, mbali na Yawe. Kwa nini wewe mufalme wa Israeli umetoka kuyatafuta maisha yangu kama mutu anayewinda kwale juu ya milima?” Halafu Saulo akajibu: “Mimi nimefanya makosa. Rudi mwana wangu Daudi. Sitakuzuru tena kwa sababu leo maisha yangu yalikuwa ya bei kali mbele yako. Mimi nimekuwa mupumbafu na nimekosa vibaya sana.” Daudi akajibu: “Ee mufalme, mukuki wako uko hapa, utume kijana wako mumoja akuje aukamate. Yawe anamulinda kila mutu kwa haki yake na uaminifu wake. Leo Yawe alikutia katika mikono yangu, lakini mimi sikunyoosha mukono wangu juu ya yule ambaye ni muchaguliwa wa Yawe. Angalia kama vile leo maisha yako yalivyokuwa na bei kali mbele yangu, ndivyo maisha yangu yapate kuwa na bei kali mbele ya Yawe; naye aniokoe kutoka taabu zote.” Saulo akamwambia Daudi: “Mungu akubariki mwana wangu Daudi. Utafanya mambo makubwa, nawe utafanikiwa katika yote.” Basi, Daudi akaenda zake; Saulo naye akarudi kwake. Daudi akajisemesha ndani ya moyo: “Siku moja, Saulo ataniangamiza. Jambo zuri kwangu ni kukimbilia katika inchi ya Wafilistini. Saulo atakata tamaa kunitafuta ndani ya mipaka ya inchi ya Israeli, nami nitakuwa salama kutoka katika mikono yake.” Kwa hiyo, mara moja Daudi na watu wake mia sita wakaenda kwa Akisi mwana wa Maoki, mufalme wa Gati. Daudi na watu wake pamoja na jamaa yake wakaishi na Akisi kule Gati. Daudi alikuwa na wake wawili: Ahinoamu kutoka Yezereheli na Abigaili mujane wa Nabali kutoka muji wa Karmeli. Saulo aliposikia kwamba Daudi amekimbilia Gati, hakumufuata tena. Siku moja, Daudi akamwambia Akisi: “Kama nimepata kukubaliwa mbele yako, ninakuomba unipe muji mumoja katika inchi yako kusudi ukuwe pahali pangu pa kuishi. Hakuna faida kwangu kuishi nawe katika muji huu wa kifalme.” Siku hiyo, Akisi akamupa muji wa Ziklagi. Kwa hiyo, tangu siku hiyo muji wa Ziklagi ukakuwa mali ya wafalme wa Yuda. Daudi aliishi katika inchi ya Wafilistini kwa muda wa mwaka mumoja na miezi mine. Katika muda huo, Daudi na watu wake waliwashambulia Wagesuri, Wagirzi na Waamaleki, ambao walikuwa wenyeji wa inchi hiyo tangu zamani. Aliwashambulia katika inchi yao mpaka Suri, hata kwa mupaka na Misri. Daudi aliipiga inchi hiyo pasipo kuacha mutu yeyote muzima, akuwe mwanaume au mwanamuke, akateka kondoo, ngombe, punda, ngamia na nguo; kisha akarudi na kufika kwa Akisi. Akisi alipomwuliza: “Leo mashambulizi yako yalikuwa juu ya nani?” Daudi alimwambia: “Juu ya Negebu ya Yuda” au “Juu ya Negebu ya Wayerameli” au “Juu ya Negebu ya Wakeni”. Daudi hakumwacha mutu yeyote muzima akuwe mwanaume au mwanamuke kusudi aletwe Gati; alifikiri ndani ya moyo: “Wanaweza kueleza juu yetu na kusema: ‘Daudi alifanya kitendo hiki na kile.’ ” Hivyo ndivyo Daudi alivyozoea kutenda wakati wote alipoishi katika inchi ya Wafilistini. Kwa hiyo, Akisi alimusadiki Daudi, akifikiri: “Wanainchi wenzake Waisraeli hawamupendi kabisa. Kwa hiyo, atanitumikia maisha yake yote.” Nyuma ya muda fulani, Wafilistini walikusanya waaskari wao tayari kwenda kupigana na Waisraeli. Akisi akamwambia Daudi: “Uelewe vizuri kwamba wewe na watu wako munapaswa kwenda pamoja nami kupigana vita.” Daudi akamujibu Akisi: “Kweli! Utaona kitu ambacho mutumishi wako anaweza kufanya.” Akisi akamwambia: “Nami nitakufanya kuwa mulinzi wangu wa pekee wa maisha.” Wakati ule, Samweli alikuwa amekwisha kufa, na Waisraeli wote walikuwa wamekwisha kumwombolezea na kumuzika katika muji wake Rama. Saulo alikuwa amewafukuza kutoka katika inchi wenye kutabiri na wachawi. Wafilistini walikusanyika na kupiga kambi yao kule Sunemi; na Saulo aliwakusanya Waisraeli wote na kupiga kambi yao kwenye mulima Gilboa. Saulo alipoona kundi la waaskari wa Wafilistini, alianza kuogopa, akaanza kutetemeka kwa hofu aliyokuwa nayo ndani ya moyo wake. Hata alipomwomba Yawe shauri, Yawe hakumujibu kwa ndoto, kwa mawe ya kupiga kura, wala kwa njia ya manabii. Halafu Saulo akawaambia watumishi wake: “Munitafutie mwanamuke ambaye anaweza kuaguza kusudi nimwendee na kumwomba shauri.” Watumishi wake wakamujibu: “Kuna mwanamuke mwaguzi mumoja kule Endori.” Basi, Saulo akajigeuza na kuvaa nguo zingine, akaenda kule pamoja na watu wake wawili. Walifika kwa yule mwanamuke usiku. Saulo akamwambia: “Unifanyie uaguzi na kunipandishia mutu yeyote nitakayekutajia.” Yule mwanamuke akamwambia: “Wewe unajua kwa hakika kwamba mufalme Saulo amewaangamiza kabisa waaguzi na wachawi wote katika inchi ya Israeli. Sasa kwa nini unaniwekea mutego wa kuninasa na kuniua?” Saulo akamwapia kwa jina la Yawe, akisema: “Kama vile Yawe anavyoishi, hakuna azabu yoyote itakayokupata kutokana na jambo hili.” Yule mwanamuke akamwuliza: “Nikupandishie nani kutoka kule?” Saulo akajibu: “Unipandishie Samweli.” Yule mwanamuke alipomwona Samweli akalalamika kwa sauti kubwa, akamwambia Saulo: “Kwa nini umenidanganya? Wewe ni Saulo!” Mufalme Saulo akamwambia: “Usiogope! Unaona nini?” Yule mwanamuke akamujibu: “Ninaona mungu akipanda toka ndani ya udongo.” Saulo akamwambia yule mwanamuke: “Ni mufano wa nani?” Yule mwanamuke akamwambia: “Mwanaume muzee anapanda juu, naye anajifunika kanzu.” Halafu, Saulo akatambua kwamba yule ni Samweli. Saulo akainama uso mpaka chini, kwa heshima. Samweli akamwambia Saulo: “Kwa nini unanisumbua kwa kunipandisha?” Saulo akamujibu: “Mimi nina taabu kubwa! Wafilistini wananishambulia kwa vita, na Mungu ameniachilia. Hanijibu tena kwa njia ya manabii wala kwa ndoto. Ndiyo maana nimekuita unijulishe kitu cha kufanya.” Samweli akasema: “Kwa nini unaniomba shauri ikiwa Yawe amekuachilia na amekuwa adui yako? Yawe amekutendea kile alichokuambia kwa njia yangu. Yawe ameurarua ufalme kutoka katika mikono yako, na amemupa Daudi jirani yako. Maana, wewe haukuitii sauti ya Yawe, wala haukuitimiza kasirani yake juu ya Waamaleki. Ndiyo maana leo Yawe amekutendea mambo haya. Zaidi ya hayo, Yawe atakutia wewe pamoja na Waisraeli wote katika mikono ya Wafilistini. Kesho, wewe na wana wako mutakuwa pamoja nami. Hata waaskari wa Israeli, Yawe atawatia katika mikono ya Wafilistini.” Kwa rafla, Saulo akiwa na hofu kutokana na maneno ya Samweli, alianguka chini. Hakukuwa na nguvu zozote kwa sababu alikuwa hajakula kitu chochote kwa siku nzima, usiku na muchana. Halafu yule mwanamuke alimwendea Saulo, na alipoona kwamba Saulo ameshikwa na hofu sana, alimwambia: “Mimi mutumishi wako nimehatarisha maisha yangu kwa kufanya kile ulichoniambia nikufanyie. Sasa, unisikilize mimi mutumishi wako. Nitakutayarishia mukate kusudi ukule nawe utakuwa na nguvu za kuendelea na safari yako.” Lakini Saulo alikataa na kusema: “Sitakula.” Lakini watumishi pamoja na yule mwanamuke, walimusihi akule, naye akawasikiliza. Kwa hiyo alisimama kutoka chini na kuikaa kwenye kitanda. Yule mwanamuke alikuwa na mwana-ngombe wake mumoja katika nyumba yake aliyenona, akamuchinja haraka, akatwaa unga wa ngano, akauponda, akatengeneza mukate usiotiwa chachu. Akamupa Saulo, akawapa vilevile watumishi wake, nao wakakula. Halafu wakaondoka na kwenda zao wakati uleule wa usiku. Wafilistini walikusanya makundi yao yote ya waaskari kule Afeki, na Waisraeli walipiga kambi kwenye chemichemi ya bonde la Yezereheli. Wakubwa watano wa Wafilistini walipokuwa wakipita na makundi yao ya waaskari ya mamia na maelfu, Daudi naye akiwa na watu wake pamoja na Akisi walikuwa wanafuata upande wa nyuma wa kundi lile. Wakubwa wa waaskari wa Wafilistini waliuliza: “Waebrania hawa wanafanya nini hapa?” Akisi akawajibu wale wakubwa wa Wafilistini: “Huyu ni Daudi, mutumishi wa Saulo mufalme wa Israeli; naye amekuwa nami kwa miaka fulani. Na tangu alipokimbilia kwangu, sijamupata na kosa lolote.” Lakini wakubwa wa Wafilistini walimukasirikia sana Akisi, wakamwambia: “Umurudishe aende pahali ulipomupa akae. Asiende hata kidogo pamoja nasi kwa vita, kama sivyo wakati wa vita atageuka na kuwa adui yetu. Hauoni kwamba mutu huyu atapata njia nzuri ya kupatana na bwana wake halafu kuwa adui yetu katika vita? Huyu ni Daudi yuleyule ambaye wanawake waliimba habari zake walipokuwa wakicheza: ‘Saulo ameua maelfu, lakini Daudi ameua maelfu kumi.’ ” Akisi akamwita Daudi na kumwambia: “Kama vile Yawe anavyoishi, umekuwa mutu wa usawa. Ingekuwa jambo zuri kwangu tuende wote katika vita, kwa maana sijaona jambo baya lolote kwako tangu siku ile ulipokuja kwangu mpaka leo hii. Hata hivyo, wakubwa hawajapendezwa nawe. Hivyo sasa, urudi kwa nyumba. Kwenda kwa amani kusudi usiwachukize wakubwa wa Wafilistini.” Daudi akamwambia Akisi: “Lakini nimefanya nini? Kama unavyosema kwamba haujaniona na kosa lolote tangu siku ile nilipoanza kukutumikia mpaka leo, kwa nini nisiende kupigana na waadui za bwana wangu mufalme?” Akisi akamwambia: “Ninajua kwamba hauna lawama mbele yangu kama malaika wa Mungu. Hata hivyo, wakubwa wa Wafilistini wamesema: ‘Asiende hata kidogo pamoja nasi katika vita’. Sasa, wewe pamoja na watumishi wa bwana wako Saulo waliokuja pamoja nawe, kesho asubui mapema, muamuke na kuondoka mara tu kunapopambazuka.” Kwa hiyo, kesho yake asubui, Daudi pamoja na watu wake waliondoka kurudi katika inchi ya Wafilistini. Lakini hao Wafilistini wakaenda Yezereheli. Kisha siku tatu, Daudi na watu wake wakarudi Ziklagi. Waamaleki walikuwa wamekwisha kushambulia Negebu pamoja na muji wa Ziklagi na kuuteketeza kwa moto. Walikuwa wameteka wanawake na watu wote waliokuwa katika muji, wakubwa kama vile wadogo. Hao waliowateka, waliondoka nao wakiwa wazima, bila kumwua mutu yeyote. Daudi na watu wake walipofika katika muji waliukuta muji umeteketezwa, na wanawake, watoto wao wanaume na wanawake wamekamatwa mateka. Halafu Daudi na watu wake wakaanza kulalamika, wakalia mpaka walipoishiwa nguvu. Wake wawili wa Daudi, Ahinoamu kutoka Yezereheli na Abigaili mujane wa Nabali, nao vilevile walikuwa wamekamatwa mateka. Sasa, Daudi alikuwa katika matatizo makubwa kwa sababu watu wake walikuwa na uchungu katika roho zao kwa kupoteza watoto wao. Kwa hiyo wakakuwa wakitaka kumupiga mawe. Lakini Daudi alijipa moyo kwa kumutegemea Yawe, Mungu wake. Daudi akamwambia kuhani Abiatari mwana wa Ahimeleki: “Uniletee kizibao cha kuhani.” Abiatari akamupelekea. Daudi akamwomba Yawe shauri: “Nikifuata kundi hili nitalikamata?” Yawe akamujibu: “Ulifuate maana utalipata na kuwaokoa hao waliotekwa.” Kwa hiyo, Daudi akaondoka pamoja na wale watu mia sita aliokuwa nao. Walipofika kwenye kijito cha Besori, wakawakuta wamoja kati ya watu waliotekwa wameachwa pale. Lakini Daudi aliendelea kulifuatilia lile kundi akiwa na watu mia ine. Watu mia mbili wakabaki pale kwa sababu walichoka sana hata hawakuweza kuvuka kijito kile. Wale watu waliokuwa na Daudi walimukuta mutu mumoja Mumisri katika jangwa, nao wakamupeleka kwa Daudi. Wakamupa mutu yule mukate na maji. Vilevile walimupa kipande cha mukate wa tini na vishada viwili vya zabibu zenye kukauka. Alipomaliza kula, akapata nguvu, maana alikuwa hajakula wala kunywa kitu chochote kwa muda wa siku tatu, muchana na usiku. Daudi akamwuliza: “Bwana wako ni nani? Na umetoka wapi?” Yeye akamwambia: “Mimi ni kijana Mumisri. Ni mutumishi wa Mwamaleki mumoja. Bwana wangu aliniacha nyuma siku tatu zilizopita kwa maana nilikuwa mugonjwa. Sisi tulishambulia Negebu ya Wakereti na eneo la Yuda pamoja na Negebu ya Kalebu. Muji wa Ziklagi tuliuteketeza kwa moto.” Daudi akamwuliza: “Utaweza kunipeleka kwenye kundi lile?” Kijana akamujibu: “Ikiwa utaniapia kwa jina la Mungu kwamba hautaniua, wala kunitia katika mikono ya bwana wangu, nitakupeleka.” Yule kijana alimwongoza Daudi mpaka kwenye kundi lile. Walipofika kule waliwakuta wanyanganyi wale wakiwa wametawanyika kila pahali maana walikuwa wakikula na kunywa kwa sababu vitu walivyonyanganya kutoka inchi ya Wafilistini na inchi ya Yuda vilikuwa vingi sana. Daudi aliwapiga tangu asubui mpaka siku ya pili magaribi. Hakuna mwanaume yeyote aliyeponyoka isipokuwa vijana mia ine ambao walipanda juu ya ngamia na kukimbia. Daudi aliokoa kila kitu Waamaleki walichokuwa wameteka, hata na wake zake wawili. Chochote kilichokuwa chao, kikuwe kikubwa au kidogo, mutoto mwanaume au mwanamuke, Daudi alikikomboa. Vilevile Daudi aliteka makundi yote ya kondoo na ngombe, na watu walioongoza nyama wale walisema: “Hivi ni vitu vya Daudi.” Daudi akawarudilia wale watu mia mbili ambao waliachwa kwenye kijito cha Besori kwa sababu walikuwa wamechoka kwa kumufuata. Wale watu walipomwona Daudi pamoja na wale waliokuwa pamoja naye, wakaenda kumupokea. Daudi alipofika karibu na watu hao, akawasalimia. Lakini watu wote waovu na wa ovyo ovyo kati ya watu waliofuatana na Daudi, wakasema: “Hatutawapa watu hawa kitu chochote tulichokikomboa maana hawakuendelea pamoja nasi. Lakini wawatwae wake zao na watoto wao, waende zao.” Daudi akawaambia: “Sivyo wandugu zangu. Hamuwezi kufanya vile kwa kile ambacho Yawe ametupatia. Alitulinda salama, na akalitia katika mikono yetu kundi lililokuja kutushambulia. Hakuna mutu atakayekubaliana na mawazo yenu! Yule aliyekwenda katika vita na yule aliyebaki na mizigo yetu, kila mutu atapewa sehemu inayolingana na ya mwenzake.” Tangu siku ile Daudi alifanya uamuzi ule kuwa sharti na agizo katika inchi ya Israeli mpaka hivi leo. Daudi aliporudia Ziklagi, aliwapelekea warafiki zake ambao ni wazee wa Yuda sehemu ya vitu akisema: “Ninawaletea zawadi kutoka katika vitu vya waadui wa Yawe.” Zawadi hizo zilikuwa kwa ajili ya wakaaji wa Beteli, wakaaji wa Ramoti katika Negebu, wakaaji wa Yatiri, wakaaji wa Aroeri, wakaaji wa Sifumoti, wakaaji wa Estemoa, wakaaji wa Rakali, wakaaji wa miji ya Wayerameli, wakaaji wa miji ya Wakeni, wakaaji wa Horma, wakaaji wa Borasani, wakaaji wa Ataki, na wakaaji wa Hebroni. Daudi aliwapelekea vilevile wakaaji wa miji yote ambako yeye na watu wake walitembelea. Basi, Wafilistini walipigana vita na Waisraeli; nao Waisraeli walikimbia mbele ya Wafilistini, na kuuawa katika mulima Gilboa. Lakini Wafilistini wakamufuatilia Saulo na wana wake, kisha wakawaua Yonatani, Abinadabu na Malki-Sua, wana wa Saulo. Vita ilikuwa kali sana upande wa Saulo. Wapiga mishale walipomwona wakamwumiza vibaya. Halafu Saulo akamwambia mutu aliyemubebea silaha: “Chomoa upanga wako unichome nikufe, kusudi watu hawa wapagani wasikuje kunichoma upanga na kunichekelea.” Lakini yule aliyemubebea silaha hakusubutu kwa sababu aliogopa sana. Kwa hiyo, Saulo alitwaa upanga wake mwenyewe, na kuuangukia. Halafu yule aliyemubebea silaha aliona kwamba Saulo amekufa, naye vilevile aliuangukia upanga wake, akakufa pamoja na Saulo. Hivi ndivyo Saulo alivyokufa na wana wake watatu, vilevile na mutu aliyemubebea silaha pamoja na watu wake wote katika siku ileile moja. Nao Waisraeli waliokuwa upande wa pili wa bonde, na wengine waliokuwa upande wa mashariki wa muto Yordani walipoona kwamba Waisraeli wamekimbia, naye Saulo na wana wake wamekufa, waliihama miji yao, wakakimbia. Wafilistini wakaenda na kukaa katika miji hiyo. Kesho yake, Wafilistini walipokwenda kutwaa vitu vya wale waliouawa, waliikuta maiti ya Saulo na wana wake kwenye mulima Gilboa. Walikata kichwa cha Saulo na kumuvua silaha zake. Halafu waliwatuma wajumbe katika inchi yao yote ya Filistia kutangaza habari njema katika nyumba ya sanamu zao na kwa watu. Zile silaha zake waliziweka katika nyumba ya Astaroti. Kisha wakautundika mwili wake kwenye ukuta wa muji wa Betisani. Lakini wakaaji wa muji wa Yabeshi-Gileadi waliposikia mambo Wafilistini waliyomutendea Saulo, mashujaa wote waliondoka, wakasafiri usiku kucha, wakaondoa mwili wa Saulo na miili ya wana wake kutoka ukuta wa Betisani, wakakuja nayo mpaka Yabesi na kuiteketeza kwa moto kule. Kisha, wakaitwaa mifupa yao na kuizika chini ya muti wa mukwaju kule Yabesi, nao wakafunga kula chakula kwa muda wa siku saba. Nyuma ya kufa kwa Saulo, Daudi alirudi kisha kuwashinda Waamaleki, akakaa Ziklagi kwa muda wa siku mbili. Siku iliyofuata, mutu mumoja kutoka kambi ya Saulo, nguo zake zikiwa zimepasuka kwa huzuni na akiwa na mavumbi juu ya kichwa, alimwendea Daudi. Alipomufikia Daudi, alijitupa uso mpaka chini mbele yake kwa heshima. Daudi akamwambia: “Unatoka wapi?” Naye akamwambia: “Nimetoroka kutoka katika kambi ya Waisraeli.” Daudi akamwambia: “Uniambie jinsi mambo yalivyokuwa kule.” Yule mutu akamujibu: “Watu wetu wameyakimbia mapigano na wengi kati yetu wameuawa. Zaidi ya hayo, Saulo na mwana wake Yonatani vile vile wameuawa.” Daudi akamwuliza yule kijana: “Unajua namna gani kwamba Saulo na mwana wake Yonatani wamekufa?” Yule kijana akamujibu: “Kwa bahati, nilikuwa juu ya mulima Gilboa. Nilimwona Saulo akiegemea mukuki wake na magari ya waaskari wapanda-farasi ya waadui zake yalikuwa yanamusonga sana. Saulo alipoangalia nyuma, aliniona, akaniita. Nilipoitika, yeye aliniuliza mimi ni nani, nami nikamwambia kwamba mimi ni Mwamaleki. Kwa hiyo, akaniambia: ‘Sogea karibu uniue maana nimeumizwa vibaya na maumivu ni makali. Lakini ningali bado muzima’. Kwa hiyo, nilikwenda karibu naye na kumwua, kwa sababu nilikuwa na uhakika kwamba akianguka chini, hataweza kuishi zaidi. Lakini taji iliyokuwa juu ya kichwa chake na kikomo kilichokuwa kwenye mukono wake, vyote nimekuletea wewe, bwana wangu.” Daudi akapasua nguo yake kwa huzuni. Hata watu waliokuwa pamoja na Daudi wakafanya vilevile. Wakaomboleza, wakalia na kufunga kula mpaka magaribi kwa ajili ya Saulo, Yonatani mwana wake, na inchi ya Waisraeli, watu wa Yawe, kwa maana wengi kati yao waliuawa katika vita. Daudi akamwuliza yule kijana aliyemupasha habari: “Unatoka wapi?” Yeye akajibu: “Mimi ni Mwamaleki, lakini ninaishi katika inchi yako kama mugeni.” Daudi akamwuliza: “Ilikuwa namna gani wewe haukuogopa kuunyoosha mukono wako na kumwua muchaguliwa wa Yawe?” Kisha, Daudi akamwita mumoja kati ya vijana wake akamwambia: “Umwue mutu huyu!” Yule kijana alimupiga yule Mwamaleki, naye akakufa. Daudi akasema: “Ubebe wewe mwenyewe lazima ya kifo chako, maana umejishuhudia wewe mwenyewe kwa kinywa chako mwenyewe ukisema: ‘Nimemwua muchaguliwa wa Yawe.’ ” Daudi aliimba maombolezo haya kwa ajili ya Saulo na mwana wake Yonatani. Daudi alisema watu wa Yuda wafundishwe maombolezo hayo, nayo yameandikwa katika kitabu cha Yaseri. Daudi aliimba: Ewe Israeli, utukufu wako umeuawa, juu ya milima yako. Angalia jinsi mashujaa walivyoanguka! Musiuambie muji wa Gati jambo lile wala katika barabara za Askeloni, kusudi wanawake wa Wafilistini wasishangilie, wabinti za wapagani wasifurahi. Enyi milima ya Gilboa, musikuwe na umande au mvua juu yenu. Wala mashamba yenu yasitoe chochote siku zote. Maana kule ngao za shujaa zilichafuliwa, ngao ya Saulo haikupakaliwa mafuta. Upinde wa Yonatani haukurudi nyuma hata kidogo, upanga wa Saulo haukurudi bure hata kidogo. Viliua wengi siku zote, Viliua mashujaa. Saulo na Yonatani, watu wema na wa kupendeza. Katika maisha na kifo hawakutengana. Walikuwa wepesi kuliko tai, wenye nguvu kuliko simba. Wanawake wa Israeli, mumulilie Saulo, aliyewavalisha nguo nyekundu za utukufu, aliyepamba nguo zenu kwa zahabu. Jinsi gani mashujaa walivyoanguka katika vita. Yonatani analala, akiwa ameuawa kwenye milima. Ninasikitika kwa ajili yako, ndugu yangu Yonatani. Umekuwa kwangu mutu wa kupendeza siku zote. Pendo lako kwangu limekuwa la ajabu, la ajabu kuliko la mwanamuke. Jinsi gani mashujaa walivyoanguka, na silaha za vita zimeangamia. Nyuma ya mambo yale, Daudi alimwomba Yawe shauri, akasema: “Niende kwenye muji mumoja kati ya miji ya Yuda?” Yawe akamwambia: “Kwenda!” Daudi akamwuliza: “Niende katika muji gani?” Yawe akamujibu: “Kwenda kwenye muji wa Hebroni.” Kwa hiyo Daudi alikwenda Hebroni, pamoja na wake zake wawili, Ahinoamu wa Yezereheli, na Abigaili, mujane wa Nabali, kutoka muji wa Karmeli. Aliwapeleka watu wake, kila mutu akiwa pamoja na jamaa yake; nao wakafanya makao yao katika miji iliyokuwa kandokando ya Hebroni. Watu wa Yuda walimwendea Daudi kule Hebroni wakamupakaa mafuta akuwe mufalme wao. Daudi aliposikia kwamba watu wa Yabesi-Gileadi ndio waliomuzika Saulo, aliwatuma watu kule Yabesi-Gileadi na ujumbe: “Yawe awabariki kwa maana mulitendea bwana wenu Saulo mema kwa kumuzika. Sasa, Yawe awatendee kwa wema na uaminifu. Nami nitawatendea vizuri kutokana na jambo mulilolitenda. Lakini mukuwe imara na mashujaa. Saulo, bwana wenu, amekufa, na watu wa Yuda wamenipakaa mafuta nikuwe mufalme wao.” Abeneri mwana wa Neri, mukubwa wa waaskari wa Saulo alikuwa amemukamata Isiboseti mwana wa Saulo na kumupeleka kule Mahanaimu. Kule, Abeneri akamusimika Isiboseti kuwa mufalme wa inchi ya Gileadi, Asheri, Yezereheli, Efuraimu na Benjamina na Israeli yote. Isiboseti alikuwa na umri wa miaka makumi ine alipoanza kuitawala Israeli, naye alitawala kwa muda wa miaka miwili. Lakini kabila la Yuda lilimufuata Daudi. Daudi alikuwa mufalme wa kabila la Yuda kwa muda wa miaka saba na nusu, makao yake yalikuwa kule Hebroni. Abeneri mwana wa Neri, pamoja na watumishi wa Isiboseti mwana wa Saulo, waliondoka Mahanaimu na kwenda Gibeoni. Yoabu mwana wa Zeruya na watumishi wengine wa Daudi, nao walitoka na kukutana na Abeneri na watu aliokuwa nao kwenye kiziwa kinachokuwa kule Gibeoni. Kikundi kimoja kikajipanga upande mumoja wa kiziwa na kingine upande mwingine. Abeneri akamwambia Yoabu: “Uwaruhusu vijana wapigane mbele yetu!” Yoabu akamujibu: “Sawa.” Halafu vijana makumi mbili na ine wakatolewa: upande wa kabila la Benjamina na Isiboseti mwana wa Saulo, vijana kumi na wawili; na upande wa Daudi, vijana kumi na wawili. Kila mumoja alimukamata adui yake kwenye kichwa, na kumuchoma upanga katika ubavu. Hivyo wote wawili wakaanguka chini, wamekufa. Kwa hiyo, pahali pale pakaitwa Shamba la Mapanga. Pahali pale pako kule Gibeoni. Vita ya siku hiyo ilikuwa kali. Abeneri na watu wa Israeli walipigwa vibaya na watu wa Daudi. Wana watatu wa Zeruya, Yoabu, Abisayi na Asaeli walikuwa pale pale. Asaeli alikuwa na mbio kama paa. Asaeli alimufuatilia Abeneri moja kwa moja bila kugeuka upande wa kuume wala kushoto. Abeneri alipoangalia nyuma na kumwona Asaeli, alimwambia: “Ni wewe Asaeli?” Yeye akamujibu: “Kweli, ni mimi.” Abeneri akamwambia: “Geukia upande wa kuume au kushoto, umukamate kijana mumoja na kutwaa vitu vyake.” Lakini Asaeli hakuacha kumufuatilia. Abeneri akamwambia Asaeli mara ya pili: “Acha kunifuatilia. Kwa nini nikuue? Nitaweza kuonana na kaka yako Yoabu?” Lakini Asaeli alikataa. Kwa hiyo Abeneri akamupiga mukuki ndani ya tumbo kinyumenyume, na mukuki huo ukatokea katika mugongo wa Asaeli. Asaeli akaanguka chini na kufa pale pale. Watu wote waliofika pahali Asaeli alipokufia, walisimama kimya. Lakini Yoabu na Abisayi walimufuatilia Abeneri. Jua lilipokuwa linatua wakafika kwenye mulima Ama, unaokuwa upande wa mashariki ya Gia, katika barabara inayokwenda katika jangwa la Gibeoni. Watu wa kabila la Benjamina wakajikusanya pamoja, wakakuwa nyuma ya Abeneri, hivyo wakaunda kikundi chao, nao wakasimama juu ya mulima. Kisha Abeneri akamwita Yoabu: “Tutapigana siku zote? Hauoni kwamba mwisho utakuwa muchungu? Utaendelea kwa muda gani bila kuwashawishi watu wako kuacha kuwafuatilia wandugu zao?” Yoabu akamwambia: “Kama vile Yawe anavyoishi, ungekuwa haujasema jambo lile, hakika watu wangu wangeendelea kuwafuatilia wandugu zao mpaka kesho asubui.” Kwa hiyo, Yoabu akapiga baragumu na watu wakaacha kuwafuatilia watu wa Israeli, wala hawakupigana zaidi. Abeneri na watu wake walipita katika bonde la Araba usiku kucha. Wakavuka Yordani, wakatembea muchana wote mpaka Mahanaimu. Yoabu aliporudi kutoka kumufuatilia Abeneri, aliwakusanya watu wake wote, akagundua kwamba watumishi kumi na tisa wa Daudi walikosekana, bila kuhesabu Asaeli. Lakini watumishi wa Daudi walikuwa wamewaua watu mia tatu makumi sita kutoka kabila la Benjamina pamoja na watu wa Abeneri. Yoabu na watu wake walipeleka mwili wa Asaeli, wakauzika kwenye kaburi la baba yake, linalokuwa kule Betelehemu. Yoabu na watu wake walitembea usiku kucha, na kulipokucha wakafika katika muji wa Hebroni. Kulikuwa vita ya muda murefu kati ya watu waliokuwa upande wa jamaa ya Saulo, na wale waliokuwa upande wa jamaa ya Daudi. Lakini Daudi alizidi kupata nguvu zaidi na zaidi, wakati upande wa Saulo ulizidi kuwa zaifu zaidi na zaidi. Wana ambao wake wa Daudi walimuzalia kule Hebroni walikuwa: Amunoni muzaliwa wake wa kwanza, mama yake aliitwa Ahinoamu wa muji wa Yezereheli; Kiliabu muzaliwa wake wa pili, mama yake alikuwa Abigaili mujane wa Nabali wa muji wa Karmeli; Abusaloma muzaliwa wake wa tatu, mama yake alikuwa Maka binti ya Talmayi mufalme wa Gesuri; Adonia muzaliwa wa ine, mama yake alikuwa Hagiti; Sefatia muzaliwa wake wa tano, mama yake alikuwa Abitali; na Itiramu muzaliwa wake wa sita, mama yake alikuwa Egla, muke wa kwanza wa Daudi. Wake wa Daudi walimuzalia wana hawa wote alipokuwa kule Hebroni. Kadiri vita ilivyoendelea kati ya jamaa ya Daudi na ile ya Saulo, Abeneri alizidi kujiimarisha katika jamaa ya Saulo. Saulo alikuwa na habara mumoja aliyeitwa Risipa, binti ya Aya. Basi, wakati mumoja, Isiboseti akamwuliza Abeneri: “Kwa nini umelala na habara ya baba yangu?” Abeneri alikasirika sana kutokana na maneno ya Isiboseti, akasema: “Unafikiri mimi ni imbwa anayeitumikia jamaa ya Yuda? Angalia, mimi nimewatendea mema jamaa ya baba yako Saulo, wandugu zake, na warafiki zake na sikukutoa kwa Daudi mpaka leo. Hata hivyo, leo hii unaniona kuwa mwenye kosa kwa ajili ya mwanamuke. Mungu aniue ikiwa sitatimiza yote ambayo Yawe alimwapia Daudi. Yawe alimwapia Daudi kwamba atauhamisha ufalme kutoka jamaa ya Saulo na kumupa yeye. Naye atatawala inchi ya Israeli na Yuda kutokea Dani mpaka Beri-Seba.” Isiboseti hakuweza kusema neno, kwa sababu alikuwa anamwogopa Abeneri. Basi, Abeneri akatuma wajumbe kwa Daudi kule Hebroni wamwambie: “Inchi hii ni mali ya nani? Fanya agano na mimi, nami nitakusaidia kuifanya Israeli yote ikuwe chini yako.” Daudi akamujibu: “Ni vizuri, nitafanya agano nawe. Lakini ninakuomba jambo moja kwamba mbele haujaniona sharti kwanza uniletee Mikali binti ya Saulo. Hapo utaniona.” Daudi vilevile alituma wajumbe kwa Isiboseti mwana wa Saulo akisema: “Unirudishie muke wangu Mikali ambaye nilimwoa kwa magovi mia moja ya Wafilistini.” Basi, Isiboseti alituma watu, wakamukamata Mikali kutoka kwa mume wake Paltieli mwana wa Laisi. Lakini Paltieli akaenda pamoja na muke wake akiwa analia njia yote mpaka kule Bahurimu. Abeneri akamwambia Paltieli: “Rudia kwako.” Naye akarudi. Abeneri alifanya mashauri na wazee wa Waisraeli, akawaambia: “Kwa muda fulani uliopita mumekuwa mukitaka Daudi akuwe mufalme wenu. Sasa, mulilete jambo hilo mbele ya watu kwa sababu Yawe alimwahidi Daudi hivi: ‘Kwa mukono wako wewe Daudi mutumishi wangu, nitawaokoa watu wangu Waisraeli kutoka Wafilistini na kutoka waadui zao wengine.’ ” Abeneri akazungumuza na watu wa kabila la Benjamina, kisha akaenda mpaka Hebroni kumwambia Daudi juu ya yale ambayo watu wote wa Israeli na kabila lote la Benjamina walipatana kutenda. Abeneri alipomwendea Daudi, alikuwa na watu makumi mbili. Daudi aliwafanyia karamu. Abeneri akamwambia Daudi: “Mimi sasa nitakwenda na kukuletea watu wote wa Israeli, wewe bwana wangu mufalme. Watakuja na kufanya agano nawe, kusudi ukuwe mufalme wao, nawe utawatawala wote kama unavyopenda.” Daudi akamwaga Abeneri aende zake, naye akaondoka kwa amani. Kisha, Yoabu pamoja na watu wa Daudi walirudi kutoka kwenye mashambulio, wakaleta vitu vingi. Lakini Abeneri hakukuwa pamoja na Daudi kule Hebroni maana Daudi alikuwa amemwaga aende zake, naye akaondoka kwa amani. Yoabu aliporudi akiwa na waaskari wake wote aliokuwa nao, aliambiwa kwamba Abeneri mwana wa Neri, alikuwa amekuja kumwona mufalme Daudi, naye amemwaga aende zake, naye ameondoka kwa amani. Yoabu alimwendea mufalme na kumwambia: “Sasa umefanya nini? Angalia Abeneri alikuja kwako; kwa nini umemwacha aende? Unajua kwamba Abeneri mwana wa Neri alikuja kukudanganya? Alikuja kusudi ajue mienendo yako na yale unayoyafanya.” Yoabu alipotoka kuzungumuza na Daudi, alituma wajumbe wamulete Abeneri, nao wakamukuta kwenye kisima cha Sira na kumurudisha, lakini Daudi hakujua jambo hilo. Abeneri aliporudi Hebroni, Yoabu alimupeleka pembeni kwenye mulango sawa vile anataka kuzungumuza naye kwa siri. Hapo Yoabu akamukata Abeneri katika tumbo kwa sababu Abeneri alikuwa amemwua ndugu yake Asaeli, na Abeneri akakufa. Nyuma ya pale Daudi aliposikia habari hizo alisema: “Mimi na ufalme wangu hatuna kosa mbele ya Yawe juu ya damu ya Abeneri mwana wa Neri. Lazima ya mauaji hayo yakuwe juu ya kichwa cha Yoabu na jamaa yote ya baba yake! Jamaa ya Yoabu isikose mutu mwenye ugonjwa wa kisonono siku zote, au ugonjwa wa ukoma, au anayetembelea kwa miti au kuuawa kwa upanga, au mwenye kukosa chakula!” Yoabu na ndugu yake Abisayi walimwua Abeneri kwa sababu alikuwa amemwua ndugu yao Asaeli wakati wa vita kule Gibeoni. Kisha, mufalme Daudi akamwambia Yoabu na wale wote waliokuwa pamoja naye, wapasue nguo zao, wavae nguo ya gunia kusudi wafanye kilio kwa ajili ya Abeneri. Wakati wa mazishi hayo, mufalme Daudi alitembea nyuma ya kipoyi cha maiti ya Abeneri. Abeneri alizikwa kule Hebroni na mufalme aliomboleza kwa sauti akiwa pembeni ya kaburi. Watu wengine wote walifanya vile vile. Mufalme alimwomboleza Abeneri akisema: “Imekufikia namna gani ee Abeneri kufa kama mupumbafu? Mikono yako haikufungwa na miguu yako haikutiwa minyororo. Amekufa kama mutu aliyeuawa na waovu!” Na watu wote walimulilia tena. Kisha, watu wote walikwenda kumusihi Daudi akule chakula wakati ulipokuwa bado muchana. Lakini Daudi aliapa akawaambia: “Mungu aniue ikiwa nitaonja chakula au kitu chochote mpaka jua litakapotua.” Watu wote waliyaona mambo hayo, nao walipendezwa; kama vile kila kitu mufalme alichofanya kilivyowapendeza. Kwa hiyo, siku ile, Waisraeli wote walielewa kwamba haikukuwa nia ya mufalme Daudi kumwua Abeneri mwana wa Neri. Mufalme Daudi aliwaambia watumishi wake: “Hamujui kwamba leo mukubwa na mutu wa heshima amekufa katika inchi ya Israeli? Ijapokuwa mumenipakaa mafuta kusudi nikuwe mufalme, lakini leo mimi ni zaifu. Hawa wana wa Zeruya ni wakali kupita kipimo. Yawe awaazibu waovu hawa sawasawa na uovu wao.” Isiboseti mwana wa Saulo, aliposikia kwamba Abeneri ameuawa kule Hebroni, alivunjika moyo na watu wote wa Israeli walifazaika. Mwana huyo wa Saulo alikuwa na watu wawili waliokuwa viongozi wa makundi yake ya waaskari. Mumoja aliitwa Bana na mwingine Rekabu. Hao walikuwa wana wa Rimoni, mutu wa kabila la Benjamina wa muji wa Beroti (kwa maana Beroti vilevile ulikuwa mali ya kabila la Benjamina). Wakaaji wa Beroti walikimbilia Gitaimu, na wameishi kule kama wageni mpaka leo. Yonatani mwana wa Saulo alikuwa na mutoto aliyekuwa kilema wa miguu. Mutoto huyo aliitwa Mefiboseti. Mefiboseti alikuwa na umri wa miaka mitano wakati habari za kifo cha Saulo na Yonatani ziliposikilika kutoka Yezereheli. Kwa wakati ule, mulezi wake aliposikia kwamba Saulo na Yonatani waliuawa kule Yezereheli, akamukamata Mefiboseti na kukimbia naye. Lakini alipokuwa anakimbia kwa haraka, mutoto huyo alianguka na kuwa kilema. Rekabu na Bana wana wa Rimoni wa Beroti wakaenda kwa nyumba ya Isiboseti. Walifika kule wakati wa jua kali ya muchana, Isiboseti alipokuwa anapumzika mwake. Halafu walikamata kichwa cha Isiboseti na kumupelekea Daudi kule Hebroni. Nao wakamwambia mufalme Daudi: “Hiki ni kichwa cha Isiboseti mwana wa Saulo ambaye ni adui yako aliyekuwa anataka kuyaangamiza maisha yako. Yawe leo amekulipizia kisasi juu ya Saulo na wazao wake.” Lakini Daudi akamujibu Rekabu na ndugu yake Bana, wana wa Rimoni wa Beroti: “Kama vile Yawe anavyoishi, yeye ameyakomboa maisha yangu kutoka kila adui. Yule mutu aliyekuja kuniambia kwamba Saulo amekufa, akizani kwamba ananiletea habari njema, nilimukamata na kumwua kule. Hivyo ikakuwa ndiyo zawadi niliyomupa kutokana na habari yake. Mutu mwovu anapomwua mutu wa haki akiwa katika kitanda ndani ya nyumba yake, basi si ni jambo la haki kwangu kumulipiza kwa sababu ya kumwanga damu kwa kumwondosha toka katika dunia?” Daudi akawaamuru vijana wake, nao wakawaua. Wakawakata mikono na miguu. Halafu wakawatundika juu ya muti pembeni ya kisima kule Hebroni. Lakini walikichukua kichwa cha Isiboseti na kukizika katika kaburi la Abeneri kule Hebroni. Kisha makabila yote ya Waisraeli yalimwendea Daudi kule Hebroni, na kumwambia: “Angalia, sisi ni mwili na damu yako. Zamani, Saulo alipokuwa mufalme wetu wewe ndiwe uliyewaongoza Waisraeli katika vita, na Yawe alikuambia: ‘Utakuwa muchungaji wa watu wangu Waisraeli; utakuwa mukubwa juu ya inchi ya Israeli.’ ” Basi, wazee wote wa Waisraeli wakamwendea mufalme Daudi kule Hebroni. Naye akafanya agano nao mbele ya Yawe, halafu wakamupakaa Daudi mafuta akuwe mufalme wa Israeli. Daudi alikuwa na umri wa miaka makumi tatu alipoanza kutawala, na alitawala kwa muda wa miaka makumi ine. Kule Hebroni, alitawala watu wa Yuda kwa muda wa miaka saba na miezi sita, na kule Yerusalema alitawala watu wa Israeli pamoja na Yuda kwa muda wa miaka makumi tatu na mitatu. Kisha mufalme na watu wake walikwenda Yerusalema kuwashambulia Wayebusi waliokuwa wenyeji wa inchi hiyo. Lakini wao wakamwambia: “Hautaingia ndani ya muji huu, maana vipofu na vilema watakufukuza.” Walimwambia hivyo maana walifikiri kwamba Daudi asingeweza kuingia katika muji ule. Hata hivyo, mufalme Daudi aliteka kikingio cha Sayuni, ni kusema muji wa Daudi. Siku hiyo, Daudi alisema: “Mutu yeyote atakayewapiga Wayebusi apitie kwenye mufereji wa maji kwa kuwashambulia vilema na vipofu ambao roho yangu inawachukia.” Ndiyo maana watu wanasema: “Vipofu na vilema hawataingia katika nyumba.” Daudi alikaa kwenye kikingio hicho. Akakiita: “Muji wa Daudi.” Daudi akaongeza muji, akianzia uwanja wa Milo kuelekea ndani. Naye Daudi akazidi kuwa na uwezo zaidi kwa sababu Yawe, Mungu wa majeshi, alikuwa pamoja naye. Kisha, mufalme Hiramu wa Tiro alituma wajumbe kwa Daudi. Alimupelekea vilevile miti ya mierezi, waseremala na wajengaji ambao walimujengea Daudi nyumba ya kifalme. Hivyo, Daudi akatambua kwamba Yawe amemwimarisha akuwe mufalme wa Israeli, na kwamba ameutukuza ufalme wake kwa ajili ya watu wake Waisraeli. Daudi alijitwalia wahabara na kuoa wake zaidi wa kule katika muji wa Yerusalema kisha kutoka Hebroni. Hao, wakamuzalia wana na wabinti. Haya ndiyo majina ya wana ambao wake zake walimuzalia kule Yerusalema: Samua, Sobabu, Natani, Solomono, Ibuhari, Elisua, Nefegi, Yafia, Elisama, Eliada na Elifeleti. Wafilistini waliposikia kwamba Daudi amepakwa mafuta kuwa mufalme wa Waisraeli, wote walitoka kwenda kumutafuta, lakini yeye alipata habari, akaingia ndani ya makimbilio. Wafilistini walifika na kujitawanya kwenye Bonde la Refaimu. Basi, Daudi alimwuliza Yawe shauri: “Niende kuwashambulia Wafilistini? Utawatia katika mikono yangu?” Naye Yawe akamwambia Daudi: “Kwenda, maana hakika nitawatia Wafilistini katika mikono yako.” Basi, Daudi akafika Bali-Perasimu na kuwashinda Wafilistini. Halafu akasema: “Yawe amepita katikati ya waadui zangu kama mafuriko ya maji yanayoenda mbio.” Kwa hiyo pahali pale pakaitwa “Bwana Anayepita Katikati”. Wafilistini waliziacha sanamu zao za miungu pahali pale, naye Daudi na watu wake wakazikamata. Kwa mara ya pili, Wafilistini walifika tena na kujitawanya kwenye bonde la Refaimu. Daudi alipomwomba Yawe shauri, Yawe alimwambia: “Usiwashambulie kutoka hapa unapokuwa, lakini zunguka nyuma yao na kuwashambulia kutokea mbele ya miti ya miforosadi. Na mara moja mutakaposikia vishindo vya miguu kwenye vilele vya miforosadi hiyo, halafu ujipe moyo maana nitakuwa nimetoka kwa kukutangulia kuwapiga waaskari wa Wafilistini.” Daudi alifanya kama vile alivyoamuriwa na Yawe, naye akawapiga Wafilistini kutokea Geba mpaka Gezeri. Kwa mara nyingine, Daudi aliwakusanya wale waaskari bora wa Israeli. Jumla yao ilikuwa watu elfu makumi tatu. Daudi aliondoka pamoja nao wote kuenda Bali-Yuda kwa kuleta Sanduku la Mungu linaloitwa kwa jina la Yawe wa majeshi, anayeikaa kwenye kiti chake cha kifalme juu ya makerubi. Basi, wakaondoa Sanduku la Mungu kutoka katika nyumba ya Abinadabu iliyokuwa juu ya mulima, wakalibeba juu ya gari jipya. Wana wa Abinadabu, Uza na Ahio, wakaongoza gari lile jipya, likiwa na Sanduku lile la Mungu, naye Ahio akiwa anatangulia mbele ya Sanduku lile. Daudi na watu wote wa Israeli, walikuwa wanaimba nyimbo na kucheza kwa nguvu zao zote, mbele ya Yawe. Walipiga ala za muziki zilizotengenezwa na muti wa muvinje: vinubi, vinanda, matari, kayamba na matoazi. Walipofika kwenye uwanja wa kupepetea ngano wa Nakoni, Uza aliunyoosha mukono wake na kuligusa Sanduku la Mungu kwa sababu wale ngombe walijikwaa. Halafu, hasira ya Yawe ikawaka juu ya Uza. Mungu akamwua palepale. Uza akakufa palepale pembeni ya Sanduku la Mungu. Naye Daudi alikasirika maana Yawe alimwazibu Uza kwa hasira. Kwa hiyo, pahali pale pakaitwa “Azabu ya Uza” mpaka hivi leo. Siku hiyo Daudi alimwogopa Yawe akasema: “Sasa Sanduku la Yawe litanifikia namna gani?” Kwa hiyo, Daudi hakukuwa tayari kwa kulipeleka Sanduku la Yawe ndani ya muji wa Daudi, lakini Daudi alilipeleka katika nyumba ya Obedi-Edomu wa Gati. Sanduku hilo la Yawe lilikaa katika nyumba ya Obedi-Edomu kwa muda wa miezi mitatu; naye Yawe akamubariki Obedi-Edomu pamoja na jamaa yake. Mufalme Daudi aliposikia kwamba Yawe ameibariki jamaa ya Obedi-Edomu na vitu vyote alivyokuwa navyo kwa sababu ya Sanduku la Mungu, akaenda kuliondoa Sanduku la Agano kutoka katika nyumba ya Obedi-Edomu na kulipeleka kwenye muji wa Daudi kwa shangwe. Watu wale waliolibeba Sanduku la Yawe kila mara walipopiga hatua sita, Daudi alitoa sadaka: ngombe dume na mwana-ngombe mumoja wenye kunona. Daudi alikuwa amejifungia kizibao cha kuhani katika kiuno chake. Alicheza kwa nguvu zake zote mbele ya Yawe. Hivyo, yeye na Waisraeli wote walilipeleka Sanduku la Yawe mpaka katika muji wa Daudi kwa shangwe na sauti kubwa ya baragumu. Sanduku la Yawe lilipokuwa linaingia katika muji wa Daudi, Mikali binti wa Saulo alichungulia kwenye dirisha, akamwona mufalme Daudi akirukaruka na kucheza mbele ya Yawe. Basi, akamuzarau ndani ya moyo wake. Kisha waliliingiza Sanduku la Yawe ndani ya hema ambalo Daudi alikuwa amelisimamisha pale na kuliweka pahali pake. Naye Daudi akatoa sadaka za kuteketezwa na sadaka za amani mbele ya Yawe. Daudi alipomaliza kutoa sadaka za kuteketezwa na za amani, aliwabariki watu kwa jina la Yawe wa majeshi, na akawagawanyia watu wote, kundi lote la Waisraeli, wanaume na wanawake, kila mumoja, mukate, kipande cha nyama na mukate wa sadaka. Kisha, watu wote waliondoka, kila mutu akarudi kwake. Daudi aliporudi kwake kwa kuibariki jamaa yake, Mikali, binti ya Saulo, alikwenda kumupokea, akasema: “Ni ajabu kwa mufalme wa Waisraeli kujiheshimu leo, kwa kujifunua uchi wake mbele ya watumishi wake na wajakazi wake sawa vile mushenzi anavyovua nguo zake mbele ya watu bila haya!” Daudi akamwambia Mikali: “Nilikuwa mbele ya Yawe ambaye alinichagua mimi pahali pa baba yako na jamaa yake, kwa kunichagua kuwa mukubwa juu ya Waisraeli, watu wa Yawe. Kwa hiyo mimi nitacheza tu mbele ya Yawe. Nitajishusha mwenyewe zaidi kuliko sasa. Wewe utaniona kuwa si kitu, lakini hao wajakazi uliowasema wataniheshimu.” Basi Mikali binti ya Saulo hakukuwa na mutoto mpaka kufa kwake. Wakati mufalme Daudi alipokuwa akikaa katika nyumba yake ya kifalme, naye Yawe amemwezesha kuwa na amani na waadui zake kila upande, mufalme Daudi akamwambia nabii Natani: “Angalia, mimi ninakaa katika nyumba iliyojengwa na miti ya mierezi, lakini Sanduku la Mungu linakaa ndani ya hema.” Natani akamwambia mufalme: “Kwenda ufanye chochote unachokifikiri ndani ya moyo wako, kwa maana Yawe yuko pamoja nawe.” Lakini usiku uleule neno la Yawe lilimufikia Natani kusema hivi: “Kwenda umwambie mutumishi wangu Daudi: Yawe anasema hivi: Si wewe utakayenijengea nyumba ya kukaa. Tangu siku ile nilipowatoa Waisraeli katika inchi ya Misri mpaka hivi leo sijaishi kwenye nyumba. Nimetembea kila pahali nikiwa ninakaa katika hema. Kila pahali ambako nimekwenda na Waisraeli wote, sikumwuliza mwamuzi yeyote wa Israeli ambaye nilimwamuru awachunge watu wa Israeli: ‘Kwa nini haujanijengea nyumba ya mierezi?’ Kwa hiyo basi, umwambie mutumishi wangu Daudi: Yawe wa majeshi anasema hivi: Nilikutoa katika shamba la malisho ya nyama ulimokuwa unawachunga kondoo, kusudi ukuwe mukubwa wa watu wangu Waisraeli. Tangu wakati ule nimekuwa pamoja nawe kokote ulikokwenda na nimewaangamiza waadui zako wote mbele yako. Nitakufanya kuwa mwenye utukufu kama wakubwa wengine katika dunia. Nami nitawachagulia watu wangu wa Israeli pahali pa kuishi niwapandikize kusudi waishi pahali pao wenyewe, wasisumbuliwe tena. Nao watu wakali hawatawatesa tena kama zamani, wakati nilipowachagua waamuzi juu ya watu wangu Waisraeli. Nami nitakulinda kutokana na waadui zako wote. Zaidi ya hayo, mimi Yawe ninakutangazia kwamba nitakujengea nyumba. “Siku zako zitakapotimia na utakapokufa na kujiunga na babu zako, nitamufanya mumoja wa watoto wako wewe mwenyewe akuwe mufalme, nami nitauimarisha ufalme wake. Yeye ndiye atakayejenga nyumba kwa ajili ya jina langu na kiti chake cha kifalme cha ufalme wake nitakiimarisha milele. Mimi nitakuwa baba yake, naye atakuwa mwana wangu. Akifanya maovu, nitamwazibu kama vile wanadamu wanavyowaazibu watoto wao kwa fimbo. Lakini sitaacha kumutendea mema yangu kama vile nilivyoacha kwa Saulo, niliyemwondoa mbele yako. Ukoo wako na ufalme wako vitadumu imara siku zote. Kiti chako cha kifalme kitakuwa imara milele.” Natani alimwelezea Daudi kila kitu ambacho alionyeshwa katika maono hayo na Mungu. Kisha mufalme Daudi akaingia ndani na kuikaa mbele ya Yawe; halafu akaomba: “Mimi ni nani, ee Bwana wangu Yawe, na jamaa yangu ni nini hata ukaniinua mpaka hapa ninapokuwa leo! Tena jambo hili lilikuwa dogo mbele ya macho yako. Zaidi ya hayo, Bwana wangu Yawe, umeahidi kuchunga jamaa yangu kwa miaka mingi inayokuja na kunijulisha hivyo, ee Bwana wangu Yawe. Nikuambie nini zaidi, mimi Daudi? Maana wewe unanijua mimi mutumishi wako, ee Bwana wangu Yawe! Kutokana na ahadi yako na kulingana na moyo wako, umetenda makubwa hayo yote kusudi unijulishe mimi mutumishi wako. Kutokana na yale tuliyosikia, wewe Yawe ni mukubwa. Hakuna anayekuwa kama wewe, na hakuna Mungu mwingine lakini wewe. Tena, hakuna watu katika dunia ambao wanaweza kufananishwa na watu wako Waisraeli. Ulikwenda kuwakomboa kutoka Misri na miungu yake kusudi wakuwe watu wako. Ukawafanyia jina na kuwatendea mambo makubwa na ya ajabu. Hata umewaimarisha watu wako Waisraeli kwa ajili yako mwenyewe, kusudi wakuwe watu wako milele; nawe ee Yawe umekuwa Mungu wao. Basi, sasa, ee Yawe Mungu, uikamilishe ile ahadi uliyosema juu yangu mimi mutumishi wako na juu ya jamaa yangu. Nalo jina lako litatukuzwa milele, nao watu watasema: ‘Yawe wa majeshi ni Mungu juu ya Israeli!’ Na jamaa yangu, mimi Daudi mutumishi wako, itaimarika mbele yako. Maana wewe, ee Yawe wa majeshi, Mungu wa Israeli, umenifunulia mimi mutumishi wako, ukisema: ‘Nitakujengea nyumba’; ndiyo maana nina uhodari wa kutoa ombi hili mbele yako. Sasa, ee Bwana wangu Yawe, wewe ndiwe Mungu, na maneno yako ni kweli. Umeniahidi mimi mutumishi wako jambo hili jema. Kwa hiyo, ninakuomba nyumba yangu mimi mutumishi wako ipate kudumu milele mbele yako. Wewe umesema. Kwa baraka zako nyumba yangu itabarikiwa milele.” Nyuma ya hayo, Daudi aliwashinda Wafilistini. Akawanyenyekeza na kunyanganya utawala wa Wafilistini. Kisha aliwashinda Wamoabu. Aliwapanga katika mistari mateka hao, na kuwalalisha chini. Aliamuru wale waliokuwa katika mistari miwili wauawe na wale wa mustari wa tatu waachwe wazima. Hivyo, Wamoabu wakakuwa watumishi wa Daudi na wakakuwa wanamulipa kodi. Daudi vilevile alimushinda Hadadezeri mwana wa Rehobu, mufalme wa Zoba. Daudi alipata ushindi huu wakati Hadadezeri alipokuwa katika njia kwenda kulirudisha eneo la muto Furati kuwa chini ya utawala wake. Daudi aliteka waaskari wapanda-farasi elfu moja na mia saba, na waaskari wa miguu elfu makumi mbili. Kisha Daudi alikata mishipa ya miguu ya nyuma ya farasi wote wa magari ya vita, lakini aliacha farasi wa kutoshelea kwa magari mia moja. Nao Waaramu wa Damasiki walipokwenda kumusaidia Hadadezeri, mufalme wa Zoba, Daudi aliwashambulia na kuwaua watu elfu makumi mbili na mbili. Halafu Daudi aliweka kambi za waaskari katika muji wa Waaramu wa Damasiki. Basi, Waaramu wakakuwa watumishi wake na wakakuwa wanamulipa kodi. Yawe alimupa Daudi ushindi kokote alikokwenda. Daudi alitwaa ngao za zahabu waaskari wa Hadadezeri walizobeba na kuzipeleka Yerusalema. Vilevile alitwaa shaba nyingi sana kutoka miji ya Beta na Berotayi, iliyokuwa miji ya Hadadezeri. Wakati Toi, mufalme wa Hamati, aliposikia kwamba Daudi amewashinda waaskari wote wa Hadadezeri, alimutuma mwana wake Yoramu kwa mufalme Daudi kwa kumupelekea salamu na shukrani kwa sababu alikuwa amepigana na Hadadezeri na kumushinda. Maana Hadadezeri alipigana na Toi mara nyingi. Yoramu alimupelekea Daudi zawadi za vyombo vya feza, zahabu na shaba. Kwa ajili ya Yawe, Daudi akatakasa zawadi zile, pamoja na feza na zahabu ambazo alikuwa ameziteka kwa mataifa yote aliyoyashinda, ni kusema Aramu, Moabu, Amoni, Filistini, Amaleki. Aliteka vilevile vitu vya mufalme Hadadezeri mwana wa Rehobu mufalme wa Zoba. Daudi alijiongezea sifa yake. Alipokuwa anarudi kisha kumushinda Hadadezeri, aliwaua Waedomu elfu kumi na nane, katika Bonde la Chumvi. Akaweka kambi za waaskari katika inchi ya Edomu yote. Nao Waedomu wote wa kule wakakuwa watumishi wake. Yawe alimupa Daudi ushindi kokote alikokwenda. Kwa hiyo, Daudi akatawala juu ya Israeli yote, naye akawahukumu watu wake wote kufuatana na haki na sheria. Yoabu mwana wa Zeruya alikuwa jemadari wa makundi yake ya waaskari. Yosafati mwana wa Ahiludi alikuwa mwandishi wa habari za kifalme. Zadoki mwana wa Ahitubu na Ahimeleki mwana wa Abiatari walikuwa makuhani. Seraya alikuwa katibu. Benaya mwana wa Yehoyada alikuwa kiongozi wa Wakereti na Wapeleti. Wana wa Daudi wakakuwa makuhani. Siku moja, Daudi aliuliza: “Hakuna hata mutu mumoja aliyebakia katika jamaa ya Saulo? Kama yuko, ningependa kumutendea mema kwa ajili ya Yonatani.” Kulikuwa mutumishi wa jamaa ya Saulo aliyeitwa Siba. Siba aliitwa kwenda kwa Daudi. Mufalme Daudi alimwuliza: “Wewe ndiwe Siba?” Naye akamujibu: “Ndiyo, mimi mutumishi wako ndiye.” Mufalme akamwuliza: “Hakuna hata mutu mumoja aliyebaki katika jamaa ya Saulo? Kama yuko, ningependa kumutendea wema wa Mungu.” Siba akamujibu: “Kuko mwana wa Yonatani. Yeye ni kilema.” Mufalme akamwuliza: “Yuko wapi?” Siba akamujibu: “Yuko kwenye nyumba ya Makiri mwana wa Amieli kule Lodebari.” Basi, mufalme Daudi akatuma watu, naye akaletwa kutoka nyumba ya Makiri mwana wa Amieli kule Lodebari. Basi, Mefiboseti mwana wa Yonatani na mujukuu wa Saulo akaenda kwa mufalme Daudi, akainama uso mpaka chini mbele ya mufalme Daudi. Daudi akamwita: “Mefiboseti!” Naye akamujibu: “Ndiyo! Mimi mutumishi wako niko hapa.” Daudi akamwambia: “Usiogope. Mimi nitakutendea mema kwa ajili ya baba yako Yonatani. Nitakurudishia yale mashamba yote yaliyokuwa ya babu yako Saulo. Nawe, utakula kwenye meza yangu siku zote.” Mefiboseti akainama, na kusema: “Mimi ni sawa na imbwa mufu. Kwa nini unishugulikie hivyo?” Kisha, mufalme Daudi akamwita Siba mutumishi wa Saulo, akamwambia: “Ile mali yote iliyokuwa ya Saulo na jamaa yake nimemupa mujukuu wa bwana wako. Wewe, watoto wako na watumishi wako mutakuwa munamulimia Mefiboseti na mutamuletea mavuno kusudi mujukuu wa bwana wako akuwe na chakula siku zote. Lakini yeye atakula kwa meza yangu.” Wakati ule, Siba alikuwa na wana kumi na watano na watumishi makumi mbili. Kisha, Siba akamwambia mufalme: “Mimi mutumishi wako, nitafanya yote kulingana na amri yako.” Basi, Mefiboseti akakuwa anapata chakula chake kwenye meza ya Daudi, kama vile mumoja wa watoto wa mufalme. Mefiboseti alikuwa na mwana mudogo aliyeitwa Mika. Watu wote wa jamaa ya Siba wakakuwa watumishi wa Mefiboseti. Kwa hiyo, Mefiboseti aliyekuwa kilema wa miguu yake yote akakuwa anaishi katika Yerusalema, na kupata chakula chake kwenye meza ya mufalme siku zote. Nyuma ya hayo, mufalme Nahasi wa Waamori akakufa, na mwana wake aliyeitwa Hanuni akakuwa mufalme pahali pa baba yake. Mufalme Daudi akasema: “Nitamutendea mema Hanuni mwana wa Nahasi kama vile baba yake alivyonitendea mimi.” Halafu, Daudi akatuma wajumbe kumupa pole kwa ajili ya kifo cha baba yake. Nao wajumbe wa Daudi walipofika katika inchi ya Waamori, wakubwa wa Waamori walimwambia bwana wao, Hanuni: “Unazani kwamba Daudi kwa kukutumia watu wa kukufariji anamuheshimu baba yako? Daudi hakuwatuma watu hawa kwako kwa kuuchunguza na kuupeleleza muji halafu wauteke?” Basi, Hanuni akawakamata wajumbe wale wa Daudi, akanyoa kila mumoja ngambo moja ya ndevu zake, akapasua nguo zao katikati mpaka kwenye matako, kisha akawaacha waende zao. Walipata haya sana kurudia kwao. Daudi alipopashwa habari, alituma watu kwa kuwapokea maana wale wajumbe walipata haya sana. Naye mufalme aliwaambia: “Mukae katika muji wa Yeriko, hata mutakapoota ndevu, kisha murudi kwa nyumba.” Waamoni walipoona kwamba wamemuchukiza Daudi, walijilipia waaskari wa miguu wa Waaramu elfu makumi mbili kutoka Beti-Rehobu na Zoba, waaskari elfu kumi na mbili kutoka Tobu, na mufalme Maka akiwa na waaskari elfu moja. Naye Daudi aliposikia habari zile, alimutuma Yoabu kwenda na kundi lote la waaskari mashujaa. Waamoni walitoka na kujipanga tayari kwa vita kwenye mulango wa muji wa Raba, muji wao mukubwa; nao Waaramu kutoka Zoba na Rehobu na watu kutoka Tobu na Maka walijipanga katika mbuga. Yoabu alipoona kwamba ilimupasa kupigana kwa upande wa mbele na nyuma, alichagua waaskari wamoja Waisraeli hodari zaidi, akawapanga mbele ya Waaramu. Wale waaskari wengine waliobaki aliwaweka chini ya uongozi wa ndugu yake Abisayi, naye akawapanga mbele ya Waamoni. Yoabu akamwambia Abisayi: “Ikiwa Waaramu wananishinda nguvu, utanisaidia lakini kama Waamoni wanakushinda nguvu, nitakuja kukusaidia. Lakini ujipe moyo! Tupigane kama wanaume kwa ajili ya watu wetu na kwa ajili ya miji ya Mungu wetu. Naye Yawe atutendee lile analoona ni jema kwake.” Basi, Yoabu na watu wake walisonga mbele kwenda kupigana na Waaramu, nao Waaramu walikimbia. Waamoni walipoona kwamba Waaramu wamekimbia, nao vilevile walimukimbia Abisayi na kuingia katika muji. Yoabu akaacha kupigana na Waamoni, akarudi Yerusalema. Lakini Waaramu walipoona kwamba wameshindwa na Waisraeli, walijikusanya pamoja. Hadadezeri aliagiza Waaramu waliokuwa ngambo ya muto Furati waletwe, wapelekwe kule Helamu wakiongozwa na Sobaki, jemadari wa waaskari wa Hadadezeri. Daudi alipopata habari, aliwakusanya pamoja waaskari wote wa Israeli, akavuka muto Yordani na kwenda mpaka Helamu. Nao Waaramu walijipanga tayari kwa vita na Daudi, wakaanza kupigana naye. Lakini Waaramu walikimbia mbele ya Waisraeli. Daudi aliwaua Waaramu mia saba waliokuwa waendeshaji wa magari ya vita, waaskari wapanda-farasi elfu makumi ine. Vilevile alimwumiza Sobaki, jemadari wa waaskari wao, naye akakufia palepale. Kisha wafalme wote waliokuwa watumishi wa Hadadezeri walipoona kwamba wameshindwa na Waisraeli, walifanya mapatano ya amani na Israeli, nao wakakuwa watumishi wa Israeli. Hivyo Waaramu hawakusubutu kuwasaidia Waamoni tena. Ilipokuwa kwa mwanzo wa mwaka mupya, wakati ambapo wafalme wanaenda kwa vita, Daudi alimutuma Yoabu na wakubwa wake pamoja na waaskari wote wa Israeli kupigana. Nao waliteka Waamoni na kushambulia muji wa Raba. Lakini Daudi alibaki Yerusalema. Siku moja, wakati wa magaribi, Daudi aliamuka toka katika kitanda, akaenda kwenye dari ya nyumba ya kifalme. Alipokuwa anatembea kule juu, alimwona mwanamuke mumoja akioga na mwanamuke yule alikuwa muzuri sana kwa umbo. Daudi akatuma mutu kuuliza mwanamuke yule ni nani. Mutu yule akamwambia Daudi: “Mwanamuke yule ni Batiseba binti ya Eliabu, na muke wa Uria wa Hiti.” Basi, Daudi alituma wajumbe wamulete. Basi Batiseba akakuja kwa Daudi, naye Daudi akalala naye. Kisha akarudi kwake. Mwanamuke yule alikuwa akitoka kujitakasa kisha ugonjwa wake wa mwezi. Mwanamuke yule akapata mimba, naye akatuma habari kwa Daudi kwamba yuko na mimba yake. Basi, Daudi akamutumia Yoabu ujumbe: “Umutume Uria wa Hiti kwangu.” Naye Yoabu akamutuma Uria kwa Daudi. Uria alipofika kwake, Daudi alimwuliza habari za Yoabu, watu wote, na hali ya vita. Halafu Daudi alimwambia Uria: “Urudie kwako unawe miguu yako.” Uria alitoka kwa mufalme, na mara moja mufalme akamupelekea zawadi. Lakini Uria hakurudi kwake. Alilala pamoja na watumishi wote wa bwana wake kwenye mulango wa nyumba ya kifalme. Daudi aliposikia kwamba Uria hakwenda kwake, Daudi akamwuliza Uria: “Wewe umetoka safari, kwa nini haukuenda kwako?” Uria alimujibu Daudi: “Sanduku la Agano, pamoja na waaskari wote wa Israeli na Yuda wanakaa kwenye vibanda katika vita. Bwana wangu Yoabu na watumishi wake wote wamepiga kambi katika mbuga. Basi ni vizuri mimi niende nikule na kunywa na kulala na muke wangu? Ninaapa kwamba, kama vile unavyoishi, sitafanya kitu cha namna ile.” Kisha, Daudi akamwambia Uria: “Basi, ukae hapa leo tena, na kesho nitakuacha urudie.” Kwa hiyo Uria akabaki katika muji wa Yerusalema siku hiyo. Siku iliyofuata, Daudi alimwalika Uria kula na kunywa kule kwake, akamulewesha Uria. Hata hivyo, usiku ule Uria hakwenda kwake, lakini alilala kwenye kilalio chake pamoja na watumishi wa bwana wake. Asubui yake, Daudi alimwandikia Yoabu barua, akamupa Uria aipeleke kwa Yoabu. Katika barua hiyo Daudi aliandika hivi: “Umuweke Uria kwenye mustari wa mbele, pahali ambako mapigano ni makali kabisa, kisha umwache kule na kurudia nyuma kusudi apigwe, na akufe.” Basi, Yoabu alipokuwa akizunguka muji, alimuweka Uria pahali ambapo alijua wazi waaskari wa waadui walikuwa hodari sana. Wakaaji wa muji ule walitoka katika muji wao na kupigana na Yoabu. Watumishi wamoja wa Daudi, waliuawa. Uria wa Hiti naye aliuawa vilevile. Kisha, Yoabu alipeleka habari zote kwa Daudi akimwelezea juu ya vita. Yoabu akamwamuru huyo mutumishi aliyemutuma hivi: “Kisha kumwelezea mufalme mambo yote juu ya vita, naye akikasirika na kukuuliza: ‘Kwa nini mulikwenda karibu na muji mulipokuwa munapigana? Hamukujua kwamba wangewapiga mishale kutoka kwenye kuta za muji wao? Nani alimwua Abimeleki mwana wa Yerubeseti? Si alikuwa mwanamuke mumoja katika muji wa Tebesi ambaye alitupa jiwe la kusagia kutoka kwenye ukuta nalo likamwua Abimeleki? Kwa nini basi, mulikwenda karibu na ukuta?’ Basi, wewe utamwambia hivi: ‘Hata mutumishi wako Uria wa Hiti, naye amekufa.’ ” Yule mujumbe alikwenda kwa Daudi na kumwambia yote ambayo aliyotumwa na Yoabu ayaseme. Yule mujumbe akamwambia Daudi: “Waadui zetu walitushinda nguvu, wakatoka inje ya miji na kutushambulia katika mbuga. Hata hivyo sisi tuliwarudisha mpaka kwenye mulango wa muji. Halafu wakatupiga mishale sisi watumishi wako kutoka juu ya ukuta. Watumishi wako wamoja waliuawa. Hata mutumishi wako Uria wa Hiti, naye amekufa.” Daudi akamwambia yule mujumbe: “Utamwambia Yoabu hivi: ‘Jambo hili lisikusumbue maana upanga hauna macho, vita inaua haizuru nani. Lakini, imarisha mashambulizi juu ya muji, mpaka uangamize muji ule’. Ndivyo utakavyomutia Yoabu moyo.” Batiseba muke wa Uria aliposikia kwamba mume wake Uria amekufa, akafanya kilio kwa ajili yake. Muda wa kufunga kilio ulipokwisha, Daudi aliagiza wamulete Batiseba na kumupeleka katika nyumba yake. Batiseba akakuwa muke wa Daudi, naye akamuzalia Daudi mutoto mwanaume. Lakini jambo hilo Daudi alilofanya lilimuchukiza Yawe. Basi Yawe akamutuma nabii Natani kwa Daudi. Natani alimwendea Daudi, akamwambia: “Kulikuwa wanaume wawili katika muji mumoja. Mumoja alikuwa tajiri na mwingine alikuwa masikini. Yule tajiri alikuwa na kondoo wengi na ngombe wengi. Lakini yule masikini alikuwa na mwana-kondoo mudogo mumoja dike, ambaye alikuwa amemununua. Alimutunza, naye akakomaa katika nyumba yake pamoja na watoto wake. Alimukulisha mwana-kondoo yule chakula kilekile kama chake na kunywea kwenye kikombe chake naye vilevile alikuwa akimukumbatia kwenye kifua. Mwana-kondoo yule alikuwa kama binti kwa yule mutu masikini. Siku moja, yule tajiri alifikiwa na mugeni. Basi, tajiri yule hakutaka kukamata kondoo mumoja kati ya kondoo wake mwenyewe au ngombe wake, amuchinjie mugeni wake, lakini alikwenda na kumunyanganya yule masikini mwana-kondoo wake, akamuchinjia mugeni wake.” Daudi aliposikia hayo, akawaka hasira juu ya yule tajiri. Akamwambia nabii Natani: “Kama vile Yawe anavyoishi, mutu aliyefanya jambo hilo anastahili kufa! Naye anapaswa kumurudishia yule masikini mwana-kondoo yule, tena mara ine, maana ametenda jambo baya na hakukuwa na huruma!” Natani akamwambia Daudi: “Wewe ndiwe mutu yule! Sasa, Yawe, Mungu wa Israeli, anasema hivi: ‘Mimi nilikupakaa mafuta ukuwe mufalme juu ya Israeli. Nilikuokoa toka katika mikono ya Saulo. Nilikupa nyumba ya bwana wako na wake zake wakuwe wako, tena nikakupa watu wa Israeli na wa Yuda uwatawale. Na kama haya yangekuwa kidogo sana kwako ningekuongezea mara mbili zaidi ya hayo. Kwa nini basi, umezarau neno langu mimi Yawe na kufanya uovu huu mbele yangu? Umemwua Uria wa Hiti kwa upanga, ukamukamata muke wake kuwa muke wako. Umewatumia Waamoni kwa kumwua Uria katika vita! Kwa hiyo basi, kwa sababu umenizarau na umemutwaa muke wa Uria wa Hiti kuwa muke wako, mauaji hayataondoka katika jamaa yako.’ Sikiliza, Yawe anasema: ‘Nitaleta hasara katika jamaa yako mwenyewe. Nitawatwaa wake zako ukiona kwa macho yako mwenyewe na kumupa jirani yako, naye atalala nao waziwazi. Wewe ulifanya jambo hilo kwa siri, lakini mimi nitayafanya hayo mbele ya Waisraeli wote waziwazi.’ ” Basi, Daudi akamwambia Natani: “Nimetenda zambi mbele ya Yawe.” Natani akamwambia: “Yawe amekusamehe zambi yako, nawe hautakufa. Hata hivyo, kwa sababu kwa tendo lako umemuzarau kabisa Yawe, mutoto wako atakufa.” Kisha Natani akarudi kwake. Yawe alimupiga mutoto ambaye Batiseba muke wa Uria alimuzalia Daudi, naye akakuwa mugonjwa. Daudi alimwomba Mungu kwa ajili ya mutoto yule. Akafunga kula chakula, akaingia ndani ya chumba chake, na usiku kucha akalala chini. Wazee wa nyumba yake walimufuata na kumusihi aamuke, lakini yeye alikataa, na hakukula chakula chochote pamoja nao. Nyuma ya juma moja, mutoto yule akakufa. Watumishi wa Daudi waliogopa kumwambia kwamba mutoto amekufa, maana walifikiri: “Mutoto yule alipokuwa angali muzima, tulizungumuza naye, lakini hakutusikiliza. Sasa, tutamwambia namna gani kama mutoto wake amekufa? Labda atajizuru.” Daudi alipowaona watumishi wake wananongonezana, akatambua kwamba mutoto wake amekufa. Kwa hiyo, akawauliza: “Mutoto amekufa?” Nao wakamujibu: “Ndiyo! Amekufa.” Kisha, Daudi akasimama, akaoga, akajipakaa mafuta na kubadilisha nguo zake. Halafu akaenda katika nyumba ya Yawe na kuabudu. Kisha akarudi kwake, akaamuru wamuletee chakula, naye akakula. Halafu watumishi wake wakamwuliza: “Ni jambo gani hili ulilofanya? Mutoto alipokuwa muzima, wewe ulifunga na kumulilia. Lakini alipokufa, ukasimama, ukakula chakula.” Daudi akawajibu: “Ni kweli mutoto alipokuwa muzima, nilifunga na kulia. Nilifanya hivyo maana nilifikiri: ‘Nani anajua? Labda Yawe atanihurumia kusudi mutoto aishi’. Lakini sasa amekufa, kwa nini nifunge? Mimi ninaweza kumurudisha katika dunia? Siku moja, nitakwenda kule alikokwenda, lakini yeye hawezi kurudi kwangu.” Halafu Daudi akamufariji Batiseba muke wake. Akalala naye, naye akapata mimba na kuzaa mutoto mwanaume, naye Daudi alimwita Solomono. Yawe alimupenda mutoto yule, naye akamutuma nabii Natani kwa Daudi kwamba amwite mutoto yule Yedidia, ni kusema “Anayependwa na Yawe”, kwa ajili ya Yawe. Wakati ule, Yoabu aliushambulia Raba muji wa Waamoni, naye akauteka muji ule wa kifalme. Yoabu akatuma ujumbe kwa Daudi: “Nimeushambulia muji wa Raba, nami nimekikamata kisima chao cha maji. Sasa uwakusanye watu wote waliobaki, upige kambi kwa kuuzunguka na kuuteka. Kama sivyo, nikiuteka, utaitwa kwa jina langu.” Kwa hiyo, Daudi akakusanya watu wote, akaenda Raba, akaushambulia na kuuteka muji ule. Kisha akatwaa taji ya mufalme wao kutoka kwenye kichwa chake. Uzito wa taji hiyo ya zahabu ulikuwa kilo makumi tatu na tano; na ndani yake mulikuwa jiwe la bei kali. Naye Daudi akavalishwa taji hiyo kwenye kichwa chake. Vilevile aliteka vitu vingi sana katika muji ule. Halafu aliwakamata watu wa muji ule, akawaweka kwa kazi ya kutumikisha misumeno, sururu za chuma, mashoka ya chuma na kuwatumia kufanya kazi katika furu ya matofali. Hivi ndivyo alivyoitendea miji yote ya Waamoni. Kisha Daudi na watu wote walirudi Yerusalema. Abusaloma mwana wa Daudi, alikuwa na dada yake muzuri sana aliyeitwa Tamari. Naye Amunoni, mwana mwingine wa Daudi, akamupenda sana Tamari. Amunoni aliteseka sana hata akajifanya mugonjwa kwa sababu ya dada yake Tamari kufuatana na vile Tamari alikuwa angali bikira, na ilionekana jambo lisilowezekana kwa Amunoni kufanya kitu chochote naye. Lakini Amunoni alikuwa na rafiki aliyeitwa Yonadabu, mwana wa Shama, ndugu ya Daudi. Yonadabu alikuwa mutu mwerevu sana. Yonadabu akamwambia Amunoni: “Wewe ni mutoto wa mufalme, kwa nini unakonda na unaonekana hauna furaha kila siku? Mbona hautaki kuniambia?” Amunoni akamwambia: “Ninamupenda Tamari, dada ya ndugu yangu Abusaloma.” Yonadabu akamwambia: “Wewe ujilalishe katika kitanda na ujifanye kuwa mugonjwa. Baba yako atakapokuja kukuona, wewe umusihi ukisema: ‘Umuruhusu dada yangu, Tamari, akuje aniletee mukate nipate kula na anitayarishie chakula mbele yangu kusudi nikione naye mwenyewe anikulishe.’ ” Kwa hiyo, Amunoni akaendelea kulala katika kitanda, akijifanya kuwa mugonjwa. Mufalme alipokwenda kumwona, Amunoni alimwambia: “Ninakuomba, Tamari akuje hapa anitengenezee mikate michache mbele yangu. Halafu yeye mwenyewe anikulishe.” Halafu, Daudi alipeleka ujumbe kwa Tamari kwamba aende kwa kaka yake Amunoni, amutengenezee chakula. Tamari alikwenda kule, akamukuta amelala. Akatwaa unga, akauponda, na kutengeneza mikate mbele ya Amunoni. Mikate hiyo ilipokuwa tayari, Tamari akaiopoa kutoka kikaango. Akamupelekea Amunoni, lakini Amunoni alikataa kula, akaamuru kwamba watu wote watoke inje, na wote wakaondoka. Kisha, Amunoni akamwambia Tamari: “Sasa uniletee mikate ile ndani ya chumba changu, halafu unikulishe.” Tamari alitwaa mikate aliyoitayarisha na kuipeleka ndani ya chumba cha kaka yake Amunoni. Hapo, alipokuwa anamupatia mikate ile, Amunoni alimukamata na kumwambia: “Kuja ulale nami.” Tamari akamwambia: “Sivyo, kaka yangu, usinilazimishe. Kitendo hiki hakifanyiki katika Israeli. Usifanye kitendo hiki cha kipumbafu. Kwa upande wangu, siwezi kuvumilia haya hiyo. Na kwa upande wako, utakuwa mumoja wa wapumbafu wa Israeli. Basi, mimi ninakusihi uzungumuze na mufalme maana hatakukataza kunioa.” Lakini Amunoni hakutaka kumusikiliza na kwa sababu alimushinda nguvu, akamukamata, akalala naye. Kisha, Amunoni akamuchukia Tamari kupita kipimo. Akamuchukia Tamari kuliko alivyomupenda zamani. Akamwambia Tamari: “Simama ondoka mara moja.” Tamari akamujibu: “Sivyo kaka yangu. Ukinifukuza utafanya ubaya mukubwa zaidi kuliko ule ulionitendea.” Lakini Amunoni hakutaka kumusikiliza. Akamwita kijana wake aliyemutumikia, akamwambia: “Umutoshe mwanamuke huyu mbele yangu. Na ufunge mulango kwa kifungio.” Amunoni na yule kijana wakamutosha inje na kufunga mulango kwa kifungio. Tamari alikuwa amevaa kanzu ndefu yenye mikono mirefu maana hivi ndivyo mabikira wa mufalme walivyovaa zamani. Basi, Tamari alijipakaa majivu kwenye kichwa, akapasua kanzu yake, akaweka mikono yake juu ya kichwa, halafu akaondoka akiwa analia kwa sauti. Kaka yake, Abusaloma, alipomwona, alimwuliza: “Kaka yako Amunoni amelala nawe? Tulia dada yangu. Yeye ni kaka yako. Usichunge jambo hilo ndani ya moyo wako.” Halafu, Tamari aliishi katika nyumba ya Abusaloma akiwa na huzuni na mwenye kutupiliwa. Mufalme Daudi aliposikia jambo hilo alikasirika sana. Abusaloma alimuchukia Amunoni sana hata hakusema naye, kwa sababu alimukamata dada yake Tamari kwa kinguvu, akalala naye. Nyuma ya miaka miwili mizima, Abusaloma alikuwa na shuguli ya kuwakata kondoo wake manyoya katika muji wa Bali-Hazori, karibu na Efuraimu. Akawaalika wana wote wa mufalme. Abusaloma alimwendea mufalme Daudi, akamwambia: “Angalia, mimi mutumishi wako ninawakata kondoo manyoya. Ninakuomba wewe mufalme pamoja na watumishi wako, muende pamoja nami, mutumishi wako.” Mufalme akamujibu: “Sivyo, mwana wangu, tusiende wote, kusudi tusikuwe muzigo kwako.” Ingawa Abusaloma alizidi kumusihi baba yake aende, lakini mufalme alikataa, lakini alimupa baraka zake. Halafu, Abusaloma akamwambia: “Kama hauendi, basi, umuruhusu ndugu yangu Amunoni tuende naye.” Mufalme akamujibu: “Lakini kwa nini aende pamoja nanyi?” Lakini Abusaloma alizidi kumusihi, na kwa mwisho mufalme akamuruhusu Amunoni na wana wake wengine waende kwenye karamu hiyo. Abusaloma akawaambia watumishi wake: “Mumwangalie Amunoni atakapokuwa amekunywa divai na kufurahi. Nitakapowaambia: ‘Mumupige Amunoni’, mumwue. Hiyo ni amri yangu kwenu. Mujipe moyo na mukuwe hodari.” Halafu, watumishi wa Abusaloma walimutendea Amunoni kama vile walivyoamriwa na Abusaloma, kisha wana wengine wa mufalme wakaondoka, kila mumoja akapanda juu ya nyumbu wake na kukimbia. Walipokuwa wangali katika njia, Daudi alipata habari kwamba Abusaloma amewaua watoto wake wote hakuna hata mumoja aliyebakia. Mufalme Daudi alisimama, akapasua nguo yake kwa huzuni akalala chini. Hata na watumishi wake wote waliokuwa wakisimama karibu naye walipasua nguo zao. Lakini Yonadabu mwana wa Simea, ndugu ya Daudi akamwambia: “Bwana wangu, usifikiri kwamba wana wako wote wameuawa. Amunoni pekee ndiye aliyeuawa. Abusaloma alikusudia kuyafanya mambo haya tangu wakati ule Amunoni alipomukamata dada yake Tamari kwa kinguvu na kulala naye. Kwa hiyo, bwana wangu, usifikiri ndani ya moyo wako kwamba watoto wako wote wamekufa. Ni Amunoni pekee ndiye aliyeuawa.” Lakini Abusaloma alikuwa amekwisha kukimbia. Naye kijana aliyekuwa na zamu ya ulinzi, akaona kundi kubwa la watu wanakuja kutokea kwenye mulima katika barabara ya kutoka Horonaimu. Yonadabu akamwambia Daudi: “Angalia mufalme, wana wako wanakuja kama nilivyokuambia mimi mutumishi wako.” Mara moja yule mutumishi alipomaliza kusema, wana wa mufalme wakaingia, wakaanza kulia kwa sauti. Mufalme na watumishi wake wote, wakalia kwa uchungu. Lakini Abusaloma alikimbilia kwa Talmayi mwana wa Amihudi, mufalme wa muji wa Gesuri. Mufalme Daudi akamufanyia mwana wake Amunoni kilio kwa siku nyingi. Abusaloma alikimbilia Gesuri, akakaa kule kwa muda wa miaka mitatu. Nyuma ya mufalme Daudi kutulia kutokana na kifo cha Amunoni, alianza kutamani kumwona mwana wake Abusaloma. Yoabu mwana wa Zeruya alitambua kwamba moyo wa Daudi ulikuwa unamwelekea Abusaloma tu. Kwa hiyo alituma watu kule Tekoa kusudi wamutafutie mwanamuke mwenye hekima. Walipomuleta, akamwambia: “Ujifanye sawa vile mwenye kuwa na kilio. Vaa nguo za kilio, usijipakae mafuta, lakini ujifanye kama mwanamuke ambaye amekuwa katika kilio kwa muda murefu. Halafu uende kwa mufalme umwambie yale ninayokuambia.” Kisha Yoabu akamwambia maneno ya kumwambia mufalme. Huyo mwanamuke kutoka Tekoa akaenda kwa mufalme, akainama uso mpaka chini mbele ya mufalme, akamwambia: “Ee mufalme, unisaidie.” Mufalme akamwambia: “Una shida gani?” Yule mwanamuke akajibu: “Ninasikitika, mimi ni mujane, mume wangu amekufa. Nilikuwa na watoto wanaume wawili. Siku moja, walipokuwa katika mbuga, walianza kugombana. Kwa vile hakukukuwa mutu yeyote wa kuwaamua, mumoja wao akamwua mwenzake. Sasa wandugu zangu wote wamenigeuka mimi mujakazi wako. Wanataka nimutoe katika mikono yao yule mutoto aliyemwua mwenzake kusudi wamwue kwa kuyaangamiza maisha ya ndugu yake. Hivyo, watamwua huyu ambaye sasa ndiye murizi. Wakifanya hivyo, watazimisha kabisa tumaini langu lililobakia, na mume wangu hataachiwa jina wala muzao katika dunia.” Mufalme akamwambia yule mwanamuke: “Rudi kwako nitaamuru jambo lako liangaliwe.” Yule mwanamuke kutoka Tekoa akasema: “Bwana wangu mufalme, makosa yote yakuwe juu yangu na juu ya jamaa ya baba yangu. Hivyo, wewe na ufalme wako musikuwe na kosa.” Mufalme akamwambia: “Mutu yeyote akikuchokoza umulete kwangu na hatakuja kukugusa tena.” Yule mwanamuke akamwambia: “Tafazali, mufalme, uniombee kwa Yawe, Mungu wako, kusudi yule ndugu yangu ambaye angelipiza kisasi kutokana na mauaji ya mwana wangu hatafanya kosa lingine kubwa la kumwua yule mutoto wangu mwingine.” Mufalme Daudi akamwambia: “Kama vile Yawe anavyoishi, hakuna hata unywele mumoja wa mwana wako utakaoanguka chini.” Yule mwanamuke akamwambia: “Ninakuomba, mimi mujakazi wako, uniruhusu niseme neno moja kwa ajili yako mufalme.” Mufalme akamwambia: “Sema”. Yule mwanamuke akamwambia: “Kwa nini basi, umepanga kutenda uovu huu juu ya watu wa Mungu? Kulingana na uamuzi wako juu ya jambo hilo, wewe mwenyewe umejihukumu kuwa na kosa kwa sababu haumuruhusu mwana wako arudi kwa nyumba kutoka kule alikokimbilia. Sisi wote tutakufa. Sisi ni kama maji yaliyomwangika chini ambayo hayawezi kuzoleka. Lakini Mungu hataki Abusaloma akufe sasa au aendelee kuishi mbali naye. Mimi nimekuja kuzungumuza nawe, bwana wangu mufalme, maana wamenitisha. Basi, mimi mujakazi wako, niliwaza kwamba ni afazali nizungumuze na mufalme, labda atanitimizia mahitaji yangu mimi mujakazi wake. Maana mufalme atanisikiliza na kuniokoa toka katika mikono ya mutu ambaye anataka kuniangamiza mimi pamoja na mwana wangu kutoka urizi wa Mungu. Nami mujakazi wako nilifikiri hivi: ‘Neno la bwana wangu mufalme litanipa amani ndani ya moyo, maana wewe bwana wangu mufalme ni kama malaika wa Mungu katika kupambanua mazuri na mabaya.’ Yawe, Mungu wako, akuwe pamoja nawe.” Halafu mufalme akamujibu yule mwanamuke: “Usinifiche jambo lolote nitakalokuuliza.” Yule mwanamuke akasema: “Sema bwana wangu mufalme.” Mufalme akamwuliza: “Haukupatana na Yoabu katika jambo hili?” Yule mwanamuke akasema: “Kama vile unavyoishi mwenyewe bwana wangu mufalme, mutu hawezi kupita pembeni juu ya jambo ulilosema bwana wangu mufalme. Yoabu yule mutumishi wako ndiye aliyenituma. Ni yeye aliyeniambia maneno yote haya niliyokuambia mimi mujakazi wako. Yoabu alifanya hivyo kwa kubadilisha mambo. Lakini, wewe bwana wangu, una hekima kama ya malaika wa Mungu hata unaweza kujua mambo yote yanayokuwa katika dunia.” Kisha, mufalme akamwambia Yoabu: “Sasa sikiliza, ninakubali shauri lako. Kwenda umurudishe yule kijana Abusaloma.” Yoabu alianguka uso mpaka chini, na kumutakia mufalme baraka, akasema: “Leo, mimi mutumishi wako, bwana wangu mufalme, ninajua kwamba nimepata kukubaliwa mbele yako, kwa kulikubali shauri langu.” Kwa hiyo, Yoabu aliondoka, akaenda Gesuri kumuleta Abusaloma katika Yerusalema. Lakini mufalme akasema: “Abusaloma aishi kwake. Asikuje hapa kuniona.” Kwa hiyo, Abusaloma akakuwa anaishi mbali, kwake na hakumwona mufalme Daudi. Katika inchi yote ya Israeli, hakuna mutu yeyote aliyesifiwa kwa uzuri wa umbo kama Abusaloma. Tangia kwenye miguu mpaka kwenye kichwa, Abusaloma hakukuwa na kilema chochote. Kila mara alipokata nywele zake, (na kila mwisho wa mwaka alikata nywele zake maana zilikuwa nzito), alipozipima, zilikuwa na uzito wa kilo mbili kulingana na vipimo vya kifalme. Abusaloma alizaa watoto watatu wanaume pamoja na binti mumoja jina lake Tamari. Tamari alikuwa na sura nzuri. Basi, Abusaloma aliishi Yerusalema kwa muda wa miaka miwili mizima bila kumwona mufalme Daudi. Kisha, Abusaloma alimutumia Yoabu ujumbe, kusudi aende kwa mufalme kwa jina lake, lakini Yoabu akakataa. Abusaloma akatuma ujumbe mara ya pili lakini Yoabu akakataa. Basi, Abusaloma akawaambia watumishi wake: “Muangalie, Yoabu ana shamba la shayiri karibu na langu. Muende mulichome kwa moto.” Kwa hiyo watumishi wa Abusaloma wakalichoma shamba la Yoabu kwa moto. Yoabu akaenda kwa Abusaloma akamwuliza: “Kwa nini watumishi wako wamechoma shamba langu?” Abusaloma akamujibu: “Nilikutumia ujumbe, ukuje huku kusudi nikutume kwa mufalme, umwulize: ‘Kwa nini niliondoka Gesuri? Ingekuwa bora kwangu kubaki kule.’ Sasa unisaidie nipate kumwona mufalme. Kama nina kosa basi, aniue!” Kwa hiyo Yoabu akaenda na kumwelezea mufalme maneno hayo yote, naye akamwita Abusaloma. Abusaloma akaingia kwa mufalme, akaanguka uso mpaka chini mbele ya mufalme. Na mufalme akamubusu Abusaloma. Nyuma ya tukio hilo, Abusaloma alijipatia gari, farasi na watu makumi tano wa kumutangulia. Abusaloma alizoea kuamuka asubui mapema na kwenda kusimama kwenye njia inayoelekea kwenye mulango wa muji. Mutu yeyote aliyekuwa na mashitaki ambayo alitaka kuyapeleka kwa mufalme kwa kupata uamuzi wake, Abusaloma alimwita mutu yule pembeni na kumwuliza: “Unatoka katika muji gani?” Kama mutu yule akisema ametoka katika muji fulani wa kabila la Waisraeli, Abusaloma alimwambia: “Maneno yako ni ya haki kabisa. Lakini hakuna mutu yeyote aliyechaguliwa na mufalme kwa kukusikiliza.” Tena, Abusaloma alimwambia: “Ingekuwa heri mimi ningekuwa mwamuzi wa Waisraeli! Kila mutu mwenye mashitaki au shauri angekuja kwangu, nami ningemupa haki yake!” Zaidi ya hayo, Abusaloma alinyoosha mukono wake akamukumbatia na kumubusu mutu yeyote aliyekuja kuinama mbele yake. Basi, hivi ndivyo Abusaloma alivyowatendea Waisraeli wote waliokuja kutafuta uamuzi wa mufalme. Kwa kufanya hivyo, Abusaloma aliiteka mioyo ya Waisraeli. Nyuma ya miaka mine, Abusaloma alimwambia mufalme: “Tafazali, uniruhusu niende kule Hebroni kwa kutimiza kiapo changu ambacho nilimwekea Yawe. Maana, mimi mutumishi wako, nilipoishi kule Gesuri katika inchi ya Aramu, nilimufanyia Yawe kiapo nikisema kama Yawe akinirudisha Yerusalema basi, nitamwabudu yeye.” Mufalme akamwambia: “Basi, kwenda kwa amani.” Abusaloma akaondoka kwenda Hebroni. Lakini Abusaloma alituma wajumbe kwa siri katika makabila yote ya Waisraeli, wakasema: “Mara moja mutakaposikia mulio wa baragumu, museme: ‘Abusaloma ni mufalme katika Hebroni!’ ” Abusaloma alipokwenda kule Hebroni, alikwenda na watu mia mbili aliowaalika kutoka Yerusalema, nao walikwenda kule kwa nia njema, wala hawakujua kitu chochote juu ya mupango wa Abusaloma. Wakati Abusaloma alipokuwa akitoa sadaka, alituma ujumbe katika muji wa Gilo kwa kumwita Ahitofeli wa muji wa Gilo, aliyekuwa mushauri wa mufalme Daudi. Uasi wa Abusaloma ukazidi kupata nguvu na watu waliojiunga naye wakazidi kuongezeka. Mujumbe mumoja akamwendea Daudi na kumwambia: “Watu wa Israeli wamevutwa na Abusaloma!” Basi, Daudi akawaambia watumishi wake waliokuwa naye Yerusalema: “Musimame tukimbie, kama sivyo, hatutaweza kumuponyoka Abusaloma. Tufanye haraka kuondoka kusudi asituletee hasara na kuuangamiza muji kwa upanga.” Watumishi wake wakamwambia: “Sisi watumishi wako, bwana wetu mufalme, tuko tayari kufanya neno lolote unaloamua.” Basi, mufalme akaondoka pamoja na jamaa yake, lakini akawaacha wahabara wake kumi wakishugulika na kazi za nyumba. Mufalme akaondoka pamoja na watu wake wote. Lakini akasimama kidogo walipofikia nyumba ya mwisho katika muji. Watumishi wote wa mufalme, Wakereti wote, Wapeleti wote, pamoja na Wagati mia sita waliomufuata mufalme Daudi kutoka muji wa Gati waliondoka pamoja naye wakimutangulia. Kisha, mufalme Daudi alipomwona Itayi wa Gati, alimwambia: “Kwa nini hata wewe umeondoka pamoja nasi? Rudi ukae na yule mufalme kijana. Maana wewe ni mugeni huku, tena ni mukimbizi kutoka kwenu. Wewe ulikuja huku juzijuzi tu. Nikufanye mutu wa kutangatanga pamoja nasi, nikijua kwamba sijui hata kule ninakokwenda? Rudi pamoja na wandugu zako. Naye Yawe akuonyeshe wema na uaminifu.” Lakini Itayi akamujibu mufalme: “Kama vile Yawe anavyoishi na kama vile bwana wangu mufalme anavyoishi, popote utakapokuwa, ikiwa ni kwa kufa au ni kwa kuishi, nami mutumishi wako nitakuwa pale.” Basi, Daudi akamwambia Itayi: “Kwenda basi, endelea mbele.” Hivyo, Itayi wa Gati akapita yeye mwenyewe pamoja na watoto wake. Daudi alipokuwa akipita pamoja na watu wake, watu wote katika inchi yote walilia kwa sauti. Mufalme Daudi akavuka kijito cha Kidroni pamoja na watu wote, wakapita kuelekea katika jangwa. Kuhani Abiatari akatoka, hata na kuhani Zadoki akatoka pamoja na Walawi wote wakilibeba Sanduku la Agano la Mungu. Wakaliweka lile Sanduku la Mungu chini, mpaka watu wote walipopita kutoka Yerusalema. Kisha mufalme akamwambia Zadoki: “Urudishe Sanduku la Agano la Mungu katika muji. Kama nimepata kukubaliwa mbele ya Yawe, bila shaka atanirudisha na kunijalia kuliona tena Sanduku lake na kuyaona makao yake. Lakini ikiwa Yawe hapendezwi nami basi, mimi niko tayari; na anitendee sawa vile anavyotaka.” Mufalme Daudi akamwambia tena Zadoki: “Twaa mwana wako Ahimasi na Yonatani mwana wa Abiatari, murudi katika muji kwa amani. Lakini nitakuwa nikingojea penye vivuko huku katika mbuga, mpaka nitakapopata habari kutoka kwako.” Kwa hiyo Zadoki na Abiatari wakalirudisha Sanduku la Agano la Mungu Yerusalema, wakabaki humo. Lakini Daudi aliendelea, akapanda kwenye mulima wa Mizeituni akilia, bila viatu na kichwa chake kimefunikwa. Hata watu wote waliokuwa pamoja naye walifunika vichwa vyao, wakapanda mulima wakilia. Wakati ule, Daudi aliambiwa kwamba hata Ahitofeli alikuwa mumoja wa waasi waliojiunga na Abusaloma. Lakini Daudi akaomba akisema: “Ee Yawe, ninakuomba uyafanye mashauri ya Ahitofeli yasifanikiwe.” Daudi alipofika kwenye kichwa cha mulima, nafasi ya kumwabudia Mungu, mutu mumoja jina lake Husai kutoka inchi ya Arki alikuja kwa kumupokea, nguo zake zikiwa zimepasuka na juu ya kichwa chake kuna mavumbi. Daudi akamwambia: “Ukienda pamoja nami, utakuwa muzigo kwangu. Urudi Yerusalema na kumwambia Abusaloma: ‘Nitakuwa mutumishi wako, ee mufalme, kama vile nilivyokuwa zamani mutumishi wa baba yako’. Kwa njia hiyo utanisaidia kupinga mashauri ya Ahitofeli. Makuhani Zadoki na Abiatari wako pamoja nawe katika muji. Basi, chochote utakachosikia kutoka katika nyumba ya mufalme, uwaambie makuhani Zadoki na Abiatari. Watoto wao wawili wanaume, Ahimasi mwana wa Zadoki na Yonatani mwana wa Abiatari, wako pamoja nao. Na neno lolote mutakalosikia mutanipasha habari kwa njia yao.” Basi, Husai, rafiki ya mufalme Daudi, akarudi katika muji wakati Abusaloma alipokuwa anaingia Yerusalema. Daudi alipokuwa ametambuka kidogo tu kichwa cha mulima, Siba mutumishi wa Mefiboseti akakuja kumupokea Daudi akiwa na punda wawili ambao walikuwa wametandikwa nao wakibeba mikate mia mbili, vishada mia moja vya zabibu yenye kukauka, matunda mia moja ya wakati wa jua na mufuko wa ngozi unaojaa divai. Mufalme akamwuliza Siba: “Kwa nini umeleta vitu hivi?” Siba akamujibu: “Punda ni kwa ajili ya kubeba watu wa jamaa yako, mikate na matunda ni kwa ajili ya vijana wote, nayo divai ni kwa ajili ya wale watakaochoka katika jangwa.” Mufalme akamwuliza: “Mwana wa bwana wako yuko wapi?” Siba akamwambia mufalme: “Yeye amebaki Yerusalema kwa sababu anazani kwamba watu wa Israeli watamurudishia ufalme wa Saulo babu yake.” Mufalme akamwambia Siba: “Basi, yale yaliyokuwa mali ya Mefiboseti sasa ni mali yako.” Siba akamwambia: “Ninashukuru, bwana wangu mufalme, nami ninaomba nipate kukubaliwa mbele yako siku zote.” Wakati Daudi alipofika kule Bahurimu, kulitokea mutu mumoja wa ukoo wa Saulo, jina lake Simei mwana wa Gera, akaanza kumulaani Daudi kwa mufululizo. Akakuwa anamutupia mufalme Daudi pamoja na watumishi wake mawe ingawa watu wengine wote na mashujaa walikuwa wakimuzunguka Daudi upande wa kuume na wa kushoto. Simei alimulaani Daudi akisema: “Kwenda! Kwenda, wewe mwuaji, mutu wa ovyoovyo! Yawe amekulipiza kisasi kutokana na kumwanga damu ya watu wote wa jamaa ya Saulo, ambaye sasa wewe umenyanganya ufalme kwa pahali pake. Sasa, Yawe amemupa mwana wako Abusaloma ufalme. Maangamizi yamekupata kwa sababu wewe ni mwuaji.” Kwa hiyo, Abisayi mwana wa Zeruya akamwambia mufalme: “Kwa nini huyu anayekuwa sawa imbwa mufu akulaani wewe bwana wangu mufalme? Uniruhusu nimwendee, nami nitakikata kichwa chake.” Lakini mufalme akamwambia: “Kuna maneno gani kati yangu na ninyi wana wa Zeruya? Ikiwa Yawe amemwambia: ‘Umulaani Daudi’, nani sasa anaweza kuuliza: ‘Kwa nini umefanya hivyo?’ ” Tena mufalme Daudi akamwambia Abisayi na hata watumishi wake wote: “Ikiwa mutoto wangu mwenyewe anayawinda maisha yangu, si ni zaidi kwa mutu wa kabila la Benjamina? Ninyi muache anilaani maana Yawe amemwagiza anilaani. Labda Yawe ataangalia mateso yangu, naye atanilipa wema kwa laana hii ninayopata leo.” Kwa hiyo, mufalme Daudi na watu wake wakaendelea na safari, naye Simei akiwa anamufuata akimutupia mawe na kurusha mavumbi juu ya mufalme Daudi. Simei alikuwa akitembea kwenye kilele cha mulima, akielekea mufalme Daudi. Kisha mufalme pamoja na watu wote waliokuwa pamoja naye, wakafika kwenye muto wakiwa wamechoka. Basi wakapumzika. Wakati ule, Abusaloma na watu wote wa Israeli wakaenda Yerusalema na Ahitofeli akiwa pamoja nao. Husayi wa inchi ya Arki, rafiki ya Daudi, akamwendea Abusaloma, akamwambia: “Uishi milele, ee mufalme! Uishi milele, ee mufalme!” Abusaloma akamwuliza Husayi: “Huu ndio uaminifu wako kwa rafiki yako Daudi? Mbona haukuenda pamoja na rafiki yako?” Husayi akamujibu: “Hapana! Maana yule ambaye amechaguliwa na Yawe, watu hawa na watu wote wa Israeli, mimi nitakuwa wake, na nitabaki naye. Zaidi ya hayo, nitamutumikia nani? Si mwana wa rafiki yangu? Basi, kama nilivyomutumikia baba yako ndivyo nitakavyokutumikia wewe.” Halafu Abusaloma alimwambia Ahitofeli: “Unipatie shauri; tufanye nini?” Ahitofeli akamwambia Abusaloma: “Ulale na wale wahabara za baba yako ambao aliwaacha kuangalia nyumba yake. Kisha watu wote wa Israeli watakaposikia kwamba umechukizwa na baba yako, hapo watu wote wanaokuwa pamoja nawe watapata nguvu.” Kwa hiyo, watu wakamupigia Abusaloma hema kwenye paa, naye akalala na wahabara za baba yake, watu wote wa Israeli wakiwa wanaona. Siku hizo, shauri lolote Ahitofeli alilotoa lilikuwa kama limetolewa na Mungu. Na shauri la Ahitofeli liliheshimiwa na Daudi na Abusaloma. Zaidi ya hayo, Ahitofeli alimwambia Abusaloma: “Uniruhusu nichague watu elfu kumi na mbili, niondoke na kumufuatia Daudi leo usiku. Nitamushambulia akiwa amechoka na amevunjika moyo, nami nitamutia hofu kubwa. Watu wote wanaokuwa pamoja naye watakimbia. Nitamwua mufalme peke yake, na kuwarudisha watu wengine wote kwako kama bibi arusi anavyorudi katika nyumba ya mume wake. Wewe unayatafuta maisha ya mutu mumoja tu na watu wengine watakuwa na amani.” Shauri hilo la Ahitofeli lilimupendeza Abusaloma na wazee wote wa Israeli. Kisha, Abusaloma akasema: “Mumwite Husayi vilevile, yule mutu wa inchi ya Arki, tusikie neno analotaka kusema.” Husayi alipofika kwa Abusaloma, Abusaloma alimwuliza: “Hivyo ndivyo Ahitofeli alivyosema. Tufanye kama vile alivyotushauria? Kama sivyo, basi, utuambie shauri lako.” Husayi akamwambia Abusaloma: “Wakati huu, shauri Ahitofeli alilolitoa si jema.” Zaidi ya hayo, Husayi akamwambia: “Wewe unajua kwamba baba yako na watu wake ni mashujaa na kwamba wamekasirikishwa kama dubu dike aliyenyanganywa watoto wake katika mbuga. Zaidi ya hayo, unajua kwamba baba yako ni bingwa wa vita. Yeye hatakaa usiku kucha pamoja na watu wake. Hata sasa amekwisha kujificha katika pango moja au nafasi ingine. Ikiwa tu katika mashambulizi ya mwanzo kunakufa watu kati yetu, habari itasambaa kwamba wafuasi wa Abusaloma wameshindwa vibaya. Watu wako watakaposikia hivyo, hata wale ambao ni hodari, wenye mioyo kama ya simba, watavunjika kabisa moyo kwa woga. Maana, Waisraeli wote wanajua kwamba baba yako ni shujaa na wote wanaokuwa pamoja naye ni watu hodari. Shauri langu ni kwamba uwakusanye kwako watu wote wa Israeli tangia Dani mpaka Beri-Seba wakuwe wengi kama muchanga wa bahari, na wewe mwenyewe peke yako uende kwa vita. Nasi tutamwendea Daudi pahali popote anapoweza kupatikana na tutamwangukia sawa vile umande unavyoanguka juu ya udongo. Basi, hakuna atakayebakia hata kama ni yeye mwenyewe au watu wake wote wanaokuwa pamoja naye. Ikiwa atakimbilia katika muji fulani, basi, watu wote wa Israeli wataleta kamba na kukokotea mawe ya majengo yake mpaka katika bonde, na hakutabaki kitu chochote hata jiwe dogo la muji ule.” Abusaloma pamoja na watu wote wa Israeli wakasema: “Shauri la Husayi ni bora kuliko shauri la Ahitofeli.” Wakakataa shauri la Ahitofeli kwa sababu Yawe alikuwa amepanga kulishinda shauri jema la Ahitofeli kusudi aweze kumuletea Abusaloma hasara. Kisha Husayi akawaambia makuhani Zadoki na Abiatari jinsi Ahitofeli na yeye mwenyewe walivyomushauria Abusaloma na wazee wa Israeli. Kisha akasema, “Mupelekee Daudi habari upesi kwamba asilale usiku kwenye vivuko katika jangwa, lakini lazima avuke muto Yordani kusudi asikamatwe na kuuawa, yeye pamoja na watu wake wote.” Wakati ule, Yonatani na Ahimasi walikuwa wakimungojea karibu na Eni-Rogeli, kusudi wasionekane na mutu yeyote wakiingia katika muji. Kila mara mujakazi fulani alikuwa akiwapelekea habari nao wakaipeleka kwa mufalme Daudi. Lakini wakati huu, walionekana na kijana mumoja ambaye alikwenda na kumupasha Abusaloma habari. Kwa hiyo, Yonatani na Ahimasi waliondoka haraka, wakaenda Bahurimu katika nyumba ya mutu fulani aliyekuwa na kisima katika kiwanja chake. Wakaingia ndani ya kisima na kujificha. Mwanamuke mwenye nyumba hiyo akatwaa kifuniko na kukifunika kisima hicho, halafu akaanika ngano juu ya kifuniko. Habari hizo hazikujulikana. Watumishi wa Abusaloma walipofika kwa yule mwanamuke, wakamwambia: “Ahimasi na Yonatani wako wapi?” Yule mwanamuke akawaambia: “Wamekwenda ngambo ya kijito.” Walipowatafuta na kuwakosa, wakarudi Yerusalema. Nyuma ya watumishi wa Abusaloma kuondoka, Yonatani na Ahimasi walitoka ndani ya kisima, wakaenda kwa mufalme Daudi na kumupasha habari. Wakamwambia: “Ondoka, uende ngambo ya muto, kwa sababu Ahitofeli amemushauria Abusaloma juu yako.” Kwa hiyo, Daudi akaondoka na watu wote waliokuwa pamoja naye, wakavuka muto Yordani. Ilipofika asubui hakuna mutu aliyebaki nyuma bila kuvuka muto Yordani. Ahitofeli alipoona kwamba shauri lake halikufuatwa, alitandika punda wake, akaenda kwake, kwenye muji wake. Alipofika kule, alipanga vizuri mambo ya nyumba yake, akajitundika. Akakufa na kuzikwa kwenye kaburi la baba yake. Basi, Daudi akaenda Mahanaimu. Abusaloma akavuka muto Yordani na watu wote wa Israeli. Wakati ule, Abusaloma alikuwa amemuweka Amasa kuwa jemadari wa waaskari pahali pa Yoabu. Amasa alikuwa mwana wa Itira, Mwisimaeli. Mama yake aliitwa Abigaili binti wa Nahasi, aliyekuwa dada ya Zeruya mama ya Yoabu. Abusaloma pamoja na watu wa Israeli walipiga kambi yao katika inchi ya Gileadi. Daudi aliwahesabu watu waliokuwa pamoja naye, akawagawanya katika vikundi vya maelfu chini ya majemadari wao na kuweka wakubwa kwa kuwaongoza; na vikundi vya mamia, navyo vikiongozwa na wakubwa wao. Daudi akatuma waaskari wake kwa vita katika vikundi vitatu: sehemu moja ya tatu ikiwa chini ya uongozi wa Yoabu, sehemu ingine ya tatu chini ya uongozi wa Abisayi mwana wa Zeruya, ndugu ya Yoabu; na sehemu ingine ya tatu chini ya uongozi wa Itayi wa muji wa Gati. Kisha mufalme Daudi akawaambia wote: “Mimi mwenyewe vilevile nitakwenda pamoja nanyi.” Lakini watu wakamwambia: “Hautakwenda. Maana, ikiwa tutakimbia, hawatajali kitu juu yetu. Ikiwa nusu yetu watakufa, hawatahangaika nasi vilevile. Lakini wewe ni wa lazima kuliko watu elfu kumi kati yetu. Kwa hiyo inafaa wewe ubaki katika muji na kutupelekea musaada ukiwa katika muji.” Mufalme akawaambia: “Nitafanya sawa vile munavyoona kuwa vizuri.” Kwa hiyo, mufalme akasimama pembeni ya mulango, nao waaskari wake wakipita: mamia na maelfu. Mufalme akawaamuru Yoabu, Abisayi na Itayi: “Kwa ajili yangu, mumutendee yule kijana Abusaloma kwa upole.” Watu wote walimusikia mufalme alipoamuru wakubwa wake juu ya Abusaloma. Kwa hiyo, waaskari wa Daudi wakaenda katika mbuga kwa kupigana na watu wa Israeli. Mapigano hayo yalifanyika katika pori la Efuraimu. Watumishi wa Daudi waliwashinda watu wa Israeli. Mauaji ya siku hiyo yalikuwa makubwa maana watu elfu makumi mbili waliuawa. Mapigano hayo yalienea katika inchi yote na watu wengi walikufa katika pori kuliko wale waliouawa kwa upanga katika vita. Kisha Abusaloma, akiwa amepanda juu ya nyumbu, alikutana na watumishi wa Daudi. Nyumbu huyo alipokuwa anapita chini ya tawi kubwa la muti wa mwalo, halafu kichwa cha Abusaloma kikakwama kwenye muti wa mwalo. Abusaloma akaachwa akilembelea katika hewa. Lakini nyumbu wake akaendelea mbele. Mutu mumoja aliyeona tukio hilo, akamwambia Yoabu: “Nimemwona Abusaloma akilembelea kwenye muti wa mwalo.” Yoabu akamwambia mutu yule: “Nini? Ulimwona Abusaloma? Kwa nini, basi, haukumupiga na kumwua palepale? Ningefurahi kukulipa vikoroti kumi vya feza na mukaba.” Lakini yule mutu akamwambia Yoabu: “Hata kama ningeuona uzito wa vikoroti elfu moja vya feza katika mukono wangu, singeunyoosha mukono wangu juu ya mwana wa mufalme kwa kumwua. Maana, tulimusikia mufalme alipokuamuru wewe Abisayi na Itayi, kwamba kwa ajili yake, mumulinde kijana Abusaloma. Kwa upande mwingine, kama ningemutendea kwa udanganyifu, hakuna lolote linalofichwa kwa mufalme. Wewe mwenyewe haungalinitetea.” Yoabu akamwambia: “Mimi sina wakati wa kupoteza pamoja nawe.” Yoabu akatwaa mikuki midogo mitatu katika mukono wake, akaenda na kumuchoma Abusaloma ndani ya moyo, Abusaloma akiwa angali muzima kwenye tawi la muti wa mwalo. Kisha, vijana kumi waliomubebea Yoabu silaha, wakakuja kumuzunguka Abusaloma, wakamupiga na kumwua. Halafu Yoabu akapiga baragumu na waaskari wote wakaacha kuwafuatilia watu wa Israeli, maana Yoabu aliwakataza. Wakamukamata Abusaloma, wakamutupia ndani ya shimo kubwa katika pori na kulundika lundo kubwa sana la mawe juu yake. Watu wote wa Israeli wakakimbia, kila mumoja kwake. Abusaloma, alipokuwa angali anaishi, alikuwa amejijengea na kujisimikia nguzo inayokuwa kwenye Bonde la Mufalme, maana alisema: “Mimi sina mutoto mwanaume wa kudumisha jina langu kusudi nikumbukwe.” Nguzo hiyo aliipa jina lake, na inaitwa “Nguzo ya Abusaloma” mpaka leo. Kisha, Ahimasi mwana wa Zadoki, akasema: “Uniruhusu nikimbie kumupelekea mufalme habari hizi kwamba Yawe amemukomboa toka katika nguvu za waadui zake.” Yoabu akamwambia: “Leo, hautapeleka habari hiyo. Unaweza kupeleka habari hizo siku nyingine. Lakini leo hautapeleka habari zozote kwa sababu mwana wa mufalme amekufa.” Halafu Yoabu akamwambia mutu mumoja wa inchi ya Etiopia: “Wewe, uende umwelezee mufalme yale uliyoona.” Mwetiopia yule akainama kwa heshima mbele ya Yoabu, akaondoka mbio. Kisha Ahimasi mwana wa Zadoki akamwambia Yoabu tena: “Si kitu; uniruhusu na mimi nimukimbilie yule Mwetiopia!” Yoabu akamwambia: “Mbona unataka kukimbia mwana wangu? Wewe hautapata zawadi yoyote kwa habari hizi!” Ahimasi akamwambia: “Si kitu; nitakimbia.” Yoabu akamwambia: “Basi, kimbia.” Kisha Ahimasi akakimbia akifuata njia ya mbuga, akamutangulia yule Mwetiopia. Daudi alikuwa ameikaa kati ya milango miwili ya muji. Naye mulinzi wa mulango akapanda juu ya ukuta mpaka juu ya mulango na alipoinua macho yake aliona mutu akikimbia peke yake. Huyo mulinzi akasema kwa sauti, akamwambia mufalme. Mufalme akasema: “Kama yuko peke yake, ni kusema ana habari.” Yule mutu akazidi kukaribia. Mulinzi akamwona mutu mwingine akikimbia, akasema tena kwa sauti kwenye mulango: “Angalia, mutu mwingine akikimbia peke yake!” Mufalme akasema: “Naye analeta habari.” Yule mulinzi akasema: “Ninaona kwamba yule anayekimbia zaidi ni Ahimasi mwana wa Zadoki.” Mufalme akasema: “Huyo ni mutu muzuri, anatuletea habari njema.” Halafu Ahimasi akamwambia mufalme kwa sauti kubwa: “Mambo yote ni sawa.” Akainama mbele ya mufalme, kwa heshima na kusema: “Yawe atukuzwe, Mungu wako, ambaye amekukomboa kutoka watu walioinua mikono yao juu yako, bwana wangu mufalme.” Mufalme akamwambia: “Kijana Abusaloma ni muzima?” Ahimasi akasema: “Wakati Yoabu aliponituma mimi mutumishi wako, niliona kulikuwa kelele nyingi, lakini sikufahamu maana yake.” Mufalme akasema: “Kaa pembeni, na usimame pale.” Basi, Ahimasi akaenda pembeni na kusimama kimya. Halafu yule Mwetiopia akafika; naye akasema: “Kuna habari njema kwako bwana wangu mufalme! Maana Yawe leo hii amekukomboa kutoka nguvu za wale wote waliokushambulia.” Mufalme akamwuliza: “Kijana Abusaloma ni muzima?” Mwetiopia akasema: “Waadui zako, bwana wangu mufalme, pamoja na wote wanaokushambulia wakikutakia mabaya, wakuwe kama huyo kijana Abusaloma.” Hapo mufalme alishikwa na huzuni kubwa, akapanda kwenye chumba kilichokuwa juu ya mulango na kulia. Alipokuwa anapanda, alilia akisema: “Mwana wangu Abusaloma, mwana wangu Abusaloma! Ingekuwa heri ningalikufa pahali pako! Ole, Abusaloma mwana wangu! Mwana wangu!” Yoabu alipata habari kwamba mufalme alikuwa akilia na kuomboleza juu ya kifo cha Abusaloma. Ushindi wa siku hiyo uligeuzwa kuwa maombolezo kwa watu wote, waliposikia kwamba mufalme anamwombolezea Abusaloma. Kwa hiyo, siku hiyo, watu waliingia katika muji kimyakimya kama watu wanaorudi katika muji wakipata haya kwa kukimbia vita. Mufalme alijifunika uso wake na kulia kwa sauti kubwa akisema: “Ole mwana wangu Abusaloma! Ole, Abusaloma, mwana wangu! Mwana wangu!” Halafu Yoabu aliingia katika nyumba ya mufalme, akamwambia: “Leo umetupatisha haya sisi watumishi wako wote ambao leo tumeyaokoa maisha yako, maisha ya watoto wako wanaume, na maisha ya watoto wako wanawake, maisha ya wake zako na maisha ya wahabara zako. Wewe unawapenda wale wanaokuchukia na unawachukia wale wanaokupenda. Umetuonyesha waziwazi leo kwamba majemadari na watumishi wako hawana maana kwako. Ninaona leo, kama Abusaloma angekuwa muzima, na sisi wote tungalikufa, ungeona ni sawa. Sasa, simama uzungumuze na watumishi wako kwa upole. Maana, ninaapa kwa Yawe, kama hauendi kuzungumuza nao, hakuna hata mumoja atakayebaki pamoja nawe leo magaribi. Hili litakuwa jambo baya zaidi kwako kuliko maovu yote yaliyokupata tangu ujana wako mpaka leo.” Kisha, mufalme akatoka, akaenda, akaikaa kwenye nafasi yake karibu na mulango. Watu wote walipoambiwa kwamba mufalme yuko kwenye mulango, wote walimwendea. Wakati ule, watu wote wa Israeli walikuwa wamekimbia, kila mumoja kwake. Watu wote walikuwa wanabishana wao kwa wao katika makabila yote ya Israeli, wakisema: “Mufalme Daudi alitukomboa toka mikono ya waadui zetu, alituokoa toka mikono ya Wafilistini. Lakini sasa ameikimbia inchi, akimukimbia Abusaloma. Tena Abusaloma ambaye tulimupakaa mafuta akuwe mufalme wetu, sasa ameuawa katika vita. Sasa, kwa nini hatuzungumuzii juu ya kumurudisha mufalme Daudi?” Mufalme Daudi akatuma ujumbe kwa makuhani Zadoki na Abiatari: “Muwaambie wazee wa Yuda: ‘Kwa nini ninyi ndio mutakuwa wa mwisho kumurudisha mufalme katika nyumba yake? Maneno yote Waisraeli waliyosema yamenifikia mimi mufalme. Ninyi ni wandugu zangu, ninyi ni damu yangu. Kwa nini mukuwe wa mwisho kunirudisha mimi mufalme kwangu? Muulize vilevile Amasa kama yeye si damu yangu. Tena Mungu aniue ikiwa simufanyi yeye kuwa jemadari wa kundi langu la waaskari tangu leo pahali pa Yoabu.’ ” Kwa hiyo, Daudi aliivuta mioyo ya watu wote wa Yuda kama mutu mumoja. Halafu, wakamupelekea ujumbe kusema: “Rudi kwako, wewe na watumishi wako wote.” Basi, mufalme akakuja kwenye muto Yordani na watu wote wa Yuda wakakuja mpaka Gilgali kwa kumupokea mufalme na kumuvukisha muto Yordani. Simei mwana wa Gera, wa kabila la Benjamina, kutoka Bahurimu, alifanya haraka kwenda pamoja na watu wengine kwa kumupokea mufalme Daudi. Simei alikwenda pamoja na watu wa kabila la Benjamina elfu moja. Siba mutumishi wa jamaa ya Saulo, pamoja na watoto wake kumi na watumishi makumi mbili, walikwenda haraka kwenye muto Yordani kumutangulia mufalme Daudi. Basi, wakavuka kwenye kivuko kwa kuisindikiza jamaa ya mufalme na kumufanyia mufalme yote aliyoyapenda. Simei mwana wa Gera akakuja, akajitupa mbele ya mufalme, akainama uso mpaka chini, wakati mufalme alipokuwa karibu kuvuka muto Yordani. Simei akamwambia mufalme: “Ninakuomba, bwana wangu mufalme, usinihesabu kuwa na kosa wala kukumbuka kosa nililofanya siku ile ulipokuwa ukiondoka Yerusalema. Ninakuomba usiyaweke hayo ndani ya moyo. Maana, mimi mutumishi wako ninajua kwamba nilitenda zambi. Hii ndiyo sababu nimekuja leo, nikiwa wa kwanza katika kabila la Yosefu kuja kukupokea wewe bwana wangu, mufalme.” Halafu Abisayi mwana wa Zeruya akasema: “Si Simei anapaswa kuuawa maana alimulaani muchaguliwa wa Yawe?” Lakini Daudi akasema: “Wana wa Zeruya, kuna maneno gani kati yangu nanyi. Kwa nini munajifanya kama waadui zangu leo? Basi inawezekana kwa mutu yeyote katika Israeli kuuawa kwa siku ya leo? Sijui kwamba mimi ni mufalme wa Israeli siku ya leo?” Kisha, mufalme akamwambia Simei: “Wewe hautauawa.” Mufalme akamwapia Simei. Mefiboseti mujukuu wa Saulo alikwenda vilevile kumupokea mufalme Daudi. Tangu siku ile mufalme alipoondoka Yerusalema mpaka wakati aliporudi salama, Mefiboseti alikuwa hajapata kunawa miguu yake, kukata ndevu zake wala hakujali kufua nguo zake. Basi, alipofika Yerusalema kwa kumupokea mufalme, Daudi alimwuliza: “Mefiboseti, kwa nini haukuandamana pamoja nami?” Mefiboseti akasema: “Ee bwana wangu mufalme, mutumishi wangu alinidanganya. Maana, mimi mutumishi wako, nilimwambia: ‘Unitandikie punda nipate kupanda juu yake kwenda pamoja na mufalme’, maana mimi mutumishi wako ni kilema. Sasa, amenisingizia kwako, ee bwana wangu mufalme. Lakini wewe, bwana wangu mufalme, uko kama malaika wa Mungu. Fanya sawa unavyotaka. Maana, jamaa yote ya babu yangu walikuwa watu ambao wamestahili kuuawa mbele yako, bwana wangu mufalme. Lakini uliniweka mimi mutumishi wako kati ya wale wanaokula kwenye meza yako. Nina haki yoyote zaidi hata nikulilie mufalme?” Mufalme akamwambia: “Usiniambie zaidi juu ya mambo yako pekee. Mimi nimekwisha amua kuwa wewe pamoja na Siba mutagawanyana inchi ya Saulo.” Lakini Mefiboseti akamwambia mufalme: “Umuruhusu Siba atwae inchi yote peke yake. Mimi nimetosheka kwamba wewe bwana wangu mufalme umerudi kwako salama.” Barzilayi wa Gileadi alikuwa amefika kutoka Rogelimu. Alikuwa amekwenda pamoja na mufalme kwenye muto Yordani kwa kumusindikiza mpaka ngambo ya muto. Barzilayi alikuwa muzee sana, mwenye umri wa miaka makumi nane. Naye Barzilayi alikuwa amemutunza mufalme alipokaa kule Mahanaimu, kwa sababu alikuwa tajiri sana. Basi, mufalme Daudi akamwambia Barzilayi: “Twende wote kule Yerusalema nami nitakutunza.” Lakini Barzilayi akamwambia mufalme: “Niko tena na miaka mingi ya kuishi ndipo niende nawe mufalme mpaka Yerusalema? Mimi leo nina umri wa miaka makumi nane. Niko na uwezo wa kutambua yanayokuwa mazuri na yale yasiyokuwa mazuri? Mimi mutumishi wako ninaweza tena kutambua onjo ya kile ninachokula au kunywa? Nitaweza tena kutambua uzuri wa sauti za waimbaji wanaume au wanawake? Kwa nini mimi mutumishi wako nikuwe muzigo wa zaidi kwako bwana wangu mufalme? Mimi mutumishi wako nitakwenda nawe mwendo mufupi ngambo ya Yordani. Kwa nini, mufalme anilipe zawadi kubwa hivyo? Ninakuomba uniruhusu mimi mutumishi wako, nikufie katika muji wangu, karibu na kaburi la baba yangu na mama yangu. Lakini huyu mutumishi wako Kimuhamu, umuruhusu aende pamoja nawe bwana wangu mufalme, na umutendee yeye lolote unaloona ni zuri.” Mufalme akamwambia: “Kimuhamu atakwenda nami, na nitamutendea lolote unaloona ni zuri. Na lolote utakalotaka nikutendee, nitakutendea.” Halafu watu wote wakavuka muto Yordani na mufalme naye akavuka. Mufalme akamubusu na kumubariki Barzilayi, na Barzilayi akarudi kwake. Mufalme aliendelea mpaka Gileadi. Kimuhamu akakuwa anafuatana naye. Watu wote wa Yuda na nusu ya watu wa Israeli walikuwa wakimusindikiza mufalme. Kisha, watu wote wa Israeli wakakuja kwa mufalme na kumwambia: “Kwa nini wandugu zetu watu wa Yuda walikuwa wamekutwaa ukiwa katika njia, wakakuvukisha muto Yordani, wewe na jamaa yako, pamoja na watu wako?” Watu wa Yuda wakawaambia watu wa Israeli: “Kwa sababu mufalme ni ndugu yetu wa karibu. Kwa nini munakasirika juu ya jambo hili? Tumekula nini wakati wowote kutoka kwake? Au yeye ametupatia zawadi yoyote?” Watu wa Israeli wakawajibu watu wa Yuda: “Tuna haki mara kumi juu ya mufalme, kuliko zile munazokuwa nazo ninyi, na hata juu ya Daudi mwenyewe. Kwa nini, basi, mulituzarau? Sisi hatukukuwa wa kwanza kusema kwamba mufalme wetu arudishwe?” Maneno ya watu wa Yuda yalikuwa makali kuliko maneno ya watu wa Israeli. Sasa ilitokea kwamba kule Gilgali kulikuwa mutu mumoja wa ovyoovyo anayeitwa Seba mwana wa Bikiri, wa kabila la Benjamina. Basi Seba alipiga baragumu, na kusema: “Hatuna ushirika wowote na Daudi; hatuna sehemu yetu katika huyo mwana wa Yese. Enyi watu wa Israeli, kila mumoja ajiendee katika hema yake!” Kwa hiyo, watu wote wa Israeli wakamwacha Daudi, wakamufuata Seba mwana wa Bikiri. Lakini watu wa Yuda walimufuata mufalme Daudi kwa uaminifu toka muto Yordani mpaka Yerusalema. Nyuma, Daudi alifika katika nyumba yake kule Yerusalema. Mufalme aliwatwaa wahabara wake kumi ambao alikuwa amewaacha kwa kuangalia nyumba yake, akawaweka kwenye nyumba moja wapate kulindwa, akawatunza vizuri, lakini hakulala nao. Kwa hiyo wahabara hao wakakuwa wakifungwa mpaka siku za kufa kwao, wakaishi kama vile walikuwa wajane. Kisha, mufalme akamwambia Amasa: “Unikusanyie watu wote wa Yuda katika siku tatu, na wewe mwenyewe ukuwe pale.” Basi, Amasa akaenda kuwaita watu wa Yuda. Lakini akachelewa kurudi katika wakati ule aliopangiwa na mufalme. Daudi akamwambia Abisayi: “Sasa, Seba mwana wa Bikiri, atatuletea taabu kuliko Abusaloma. Twaa watumishi wangu, umufuate Seba kusudi asiingie kwenye miji yenye kuta na kuponyoka tusimwone tena.” Abisayi akatoka akiwa pamoja na Yoabu, Wakereti na Wapeleti pamoja na mashujaa wote. Hao wote waliondoka Yerusalema kwenda kumufuata Seba mwana wa Bikiri. Walipofika kwenye jiwe kubwa linalokuwa kule Gibeoni, Amasa akatoka kwenda kuwapokea. Yoabu alikuwa akivaa nguo ya kiaskari, na ndani ya nguo ile kulikuwa mukaba ulioshikilia upanga kwenye kiuno chake ukiwa kwenye mufuko wake. Yoabu alipokuwa anakaribia, upanga wake ulichomoka ndani ya mufuko ukaanguka chini. Yoabu akamwambia Amasa: “Habari gani ndugu yangu?” Yoabu akamushika Amasa kwenye kidevu kwa mukono wa kuume sawa vile anataka kumubusu. Lakini Amasa hakuona upanga uliokuwa katika mukono wa Yoabu. Basi, Yoabu akamuchoma Amasa upanga ndani ya tumbo, matumbotumbo yake yakatoka inje, akakufa. Yoabu hakumuchoma upanga mara mbili. Kisha, Yoabu na ndugu yake Abisayi wakaendelea kumufuatilia Seba mwana wa Bikiri. Mutu mumoja wa Yoabu akakuja akasimama karibu na mwili wa Amasa, akasema: “Yeyote anayemupenda Yoabu na yeyote anayemupenda Daudi, amufuate Yoabu!” Amasa alikuwa bado anagaagaa ndani ya damu yake katikati ya barabara kubwa. Kwa hiyo, kila mutu aliyepita pale, alipomwona, alisimama. Lakini yule mutu alipoona kwamba watu wote walikuja na kusimama pale, aliuondoa mwili wa Amasa ndani ya barabara, akaupeleka katika shamba na kuufunika kwa nguo. Amasa alipoondolewa kwenye barabara kubwa, watu wote sasa waliendelea kumufuata Yoabu kwa kumufuatilia Seba mwana wa Bikiri. Seba alipita katika makabila yote ya Israeli mpaka katika muji wa Abeli wa Beti-Maka. Watu wote wa ukoo wa Bikiri wakakusanyika na kumufuata. Watu wote waliokuwa pamoja na Yoabu wakaenda kumuzunguka Seba akiwa katika muji ule wa Abeli wa Beti-Maka. Walilundika udongo kwa kuzunguka muji, na makimbilio. Halafu wakaanza kuubomoa ukuta kwa kuuangusha chini. Kisha, mwanamuke mumoja mwenye hekima alisikilika kutoka muji akisema: “Musikie! Musikie! Mumwambie Yoabu akuje nizungumuze naye.” Yoabu akaenda karibu naye, huyo mwanamuke akamwambia: “Wewe ndiwe Yoabu?” Yoabu akasema: “Ndiyo! Ni mimi.” Yule mwanamuke akamwambia: “Unisikilize mimi mujakazi wako.” Yoabu akamwambia: “Ninasikiliza.” Yule mwanamuke akamwambia: “Zamani watu walikuwa wakisema: ‘Muache waombe shauri kutoka muji wa Abeli’. Ndivyo watu walivyoweza kutatua matatizo. Mimi ni mumoja wa wale wanaopenda amani na uaminifu katika Israeli. Sasa wewe unakusudia kuuharibu muji ambao ni sawa vile katika Israeli. Kwa nini sasa unataka kuuangamiza muji unaokuwa mali ya Yawe?” Yoabu akamujibu: “Hata kidogo katika maisha yangu! Sina nia ya kuangamiza wala kuharibu. Ulivyosema si kweli! Lakini mutu mumoja kutoka sehemu ya milima ya Efuraimu anayeitwa Seba mwana wa Bikiri anataka kumwasi mufalme Daudi. Mumutoe kwangu nami nitaondoka katika muji wenu.” Yule mwanamuke akamwambia Yoabu: “Kichwa chake kitarushwa kwako kupitia juu ya ukuta.” Kisha, huyo mwanamuke akaenda kwa watu wote katika muji kwa hekima yake. Wakamukata Seba mwana wa Bikiri kichwa, wakakitupa inje kwa Yoabu. Kwa hiyo, Yoabu akapiga baragumu na kuwatawanya watu wake kutoka muji ule wa Abeli. Kila mutu akaenda kwake. Yoabu akarudi kwa mufalme Daudi, kule Yerusalema. Sasa Yoabu alikuwa jemadari wa waaskari wote wa Waisraeli. Benaya mwana wa Yehoyada alikuwa jemadari wa Wakereti na Wapeleti. Adoramu alikuwa musimamizi wa kazi za kulazimishwa. Yeosafati alikuwa mwandishi wa habari za kifalme. Sewa alikuwa katibu. Zadoki na Abiatari walikuwa makuhani. Ira wa muji Yairi alikuwa vilevile kuhani wa Daudi. Wakati mumoja katika siku za utawala wa Daudi kukatokea njaa kali katika inchi. Njaa hiyo ilidumu miaka mitatu yenye kufuatana. Daudi alimwomba Yawe shauri. Yawe akamwambia: “Saulo na jamaa yake wana makosa ya kumwanga damu kwa sababu aliwaua Wagibeoni.” Kwa hiyo, mufalme Daudi akawaita Wagibeoni. Wagibeoni hawakukuwa Waisraeli lakini walikuwa mabaki ya Waamori. Watu wa Israeli walikuwa wameapa kuwaacha wazima, lakini Saulo alijaribu kuwaua wote maana alikuwa na bidii ya upendeleo kwa watu wa Israeli na wa Yuda. Daudi akawauliza Wagibeoni: “Niwatendee nini? Nitalipa namna gani maovu muliyotendewa kusudi mupate kuibariki inchi hii na watu wa Yawe?” Wagibeoni wakamwambia: “Maneno kati yetu na Saulo pamoja na jamaa yake si jambo la kulipwa feza au zahabu, wala si jambo la kuua mutu yeyote katika inchi ya Israeli.” Mufalme akawauliza tena: “Sasa munasema niwatendee nini?” Wao wakamwambia mufalme: “Saulo alikusudia kutuua sisi na kutuangamiza kusipate kubakia mutu yeyote wetu popote katika eneo lolote la Israeli. Basi, utupatie watu saba kati ya wazao wake, nasi tuwatundike mbele ya Yawe juu ya mulima Gibea, kwa Saulo aliyechaguliwa na Yawe.” Mufalme akasema: “Nitawapatia nao.” Mufalme alimwacha Mefiboseti mwana wa Yonatani kwa sababu ya kiapo ambacho Daudi na Yonatani mwana wa Saulo walikuwa wamefanya kati yao kwa jina la Yawe. Lakini mufalme aliwatwaa wana wawili ambao Risipa binti ya Ahiya alimuzalia Saulo, nao ni: Armoni na Mefiboseti. Aliwatwaa vilevile watoto wote watano wanaume wa Mikali binti ya Saulo ambao alimuzalia Adrieli mwana wa Barzilayi wa muji Mehola. Daudi aliwatoa watoto hao saba wanaume kwa Wagibeoni, nao wakawatundika kwenye mulima mbele ya Yawe, wote saba wakakufa pamoja. Watoto hao waliuawa kwa mwanzo wa mavuno ya Shayiri. Kisha, Risipa binti ya Aya alitwaa nguo ya gunia, akajitandikia juu ya jiwe kubwa. Alikaa pale tangu mwanzo wa mavuno mpaka wakati wa mvua ulipofika na kuinyeshea maiti. Wakati huo wote, aliwafukuza ndege na wanyama wa pori, usiku na muchana, kusudi wasifikie maiti hizo. Daudi alisikia yale Risipa binti ya Aya, habara ya Saulo aliyofanya. Alikwenda na kuitwaa mifupa ya Saulo na ya mwana wake Yonatani kutoka kwa wakaaji wa Yabeshi-Gileadi, waliokuwa wameiiba kutoka kule Beti-Sani, ambako Wafilistini walikuwa wamemutundika Saulo na Yonatani siku ile walipomwua Saulo kwenye mulima Gilboa. Daudi akairudisha mifupa ya Saulo na ya mwana wake Yonatani kutoka kule; na kisha wakakusanya mifupa ya vijana saba waliotundikwa. Basi, watu wa Daudi wakaizika mifupa ya Saulo na ya mwana wake Yonatani katika inchi ya Benjamina, kule Zela katika kaburi la Kisi baba ya Saulo. Walifanya kila kitu ambacho mufalme aliamuru. Nyuma ya hayo, Yawe akayakubali maombi kwa ajili ya inchi. Kisha Wafilistini walifanya vita tena na Waisraeli. Daudi na watu wake wakaenda kupigana na Wafilistini. Daudi alichoka sana siku ile. Isibi-Benobi, mutu mumoja wa wazao wa majitu ambaye mukuki wake wa shaba ulikuwa na uzito wa karibu kilo tatu na nusu na aliyekuwa amejifungia upanga mupya, alisema atamwua Daudi. Lakini Abisayi mwana wa Zeruya alikwenda kumusaidia Daudi. Abisayi alimushambulia yule Mufilistini na kumwua. Kwa hiyo, watu wakamwapia Daudi wakisema: “Hautakwenda tena nasi katika vita, kusudi usiizime taa ya ufalme katika Israeli.” Nyuma ya hayo, kulitokea tena mapigano na Wafilistini kule Gobu. Kule, Sibekayi wa muji wa Husa alimwua Safu aliyekuwa mutu mumoja wa wazao wa Rafa. Kulitokea tena mapigano na Wafilistini kule Gobu. Elihanani mwana wa Yare-Oregimu, wa muji wa Betelehemu, alimwua Goliati wa muji wa Gati, ambaye mupini wa mukuki wake ulikuwa kama muti wa mufumaji wa nguo. Kisha kulitokea tena vita kule Gati ambako kulikuwa na mutu mumoja alikuwa murefu sana, na mwenye vidole sita katika kila mukono, na vidole sita katika kila muguu, jumla ya vidole vyake ilikuwa makumi mbili na ine. Yeye vilevile alikuwa wa uzao wa majitu. Alipowachekelea Waisraeli, Yonatani mwana wa Simei, ndugu ya Daudi, alimwua. Hao wane walikuwa wazao wa majitu kule Gati, nao waliuawa na Daudi pamoja na watumishi wake. Daudi alimwimbia Yawe wimbo huu siku ile Yawe alipomukomboa toka katika mikono wa waadui zake, na toka katika mukono wa Saulo. Alisema: Yawe ni: kikingio changu, kimbilio langu, mukombozi wangu, Mungu wangu, yule ambaye ninamukimbilia, ngao yangu, nguvu ya wokovu wangu, munara wangu, kimbilio langu. Mwokozi wangu, unaniokoa kutoka watesaji wakali! Ninamwita Yawe anayestahili sifa anisaidie, nami ninaokolewa kutoka kwa waadui zangu. Mawimbi ya kifo yalinizunguka, mafuriko ya maangamizi yalinishambulia, kamba za kuzimu zilinizunguka, mitego ya kifo ilikuwa mbele yangu. Katika taabu yangu, nilimwita Yawe; nilimwita Mungu wangu. Toka katika hekalu lake alisikia sauti yangu; kilio changu kilifika katika masikio yake. Halafu, dunia ikatetemeka na kutikisika, misingi ya mbinguni ikayumbayumba na kuruka, kwa maana Mungu alikuwa amekasirika. Moshi ulifuka kutoka katika pua yake, moto wenye kuteketeza ukatoka katika kinywa chake, makaa ya moto yakatokea. Aliinamisha anga, akashuka chini, na wingu jeusi lilikuwa chini ya miguu yake. Alipanda juu ya kerubi na kuruka; akaruka juu ya mabawa ya upepo. Alijifunika giza pande zote; kifuniko chake kilikuwa mawingu mazito ya mvua. Umeme ulimetameta mbele yake, makaa ya moto yakawaka. Yawe alinguruma kutoka mbinguni; Mungu Mukubwa akatoa sauti yake. Aliwapiga waadui mishale, akawatawanya; alirusha umeme, akawakimbiza. Yawe alipovikaripia, pumzi ya pua yake ilifunua vilindi vya bahari na misingi ya dunia ikaonekana. Mungu alinyoosha mukono wake kutoka juu, akanitwaa, alininyanyua kutoka ndani ya maji mengi. Aliniokoa kutoka adui yangu mwenye nguvu, kutoka hao walionichukia na kuwa na nguvu kunishinda. Walinishambulia nilipokuwa katika taabu, lakini Yawe alinikinga. Alinileta, akaniweka kwenye nafasi ya usalama; aliniponyesha kwa sababu alipendezwa nami. Yawe alinitendea kwa kadiri ya haki yangu; alinilipa kwa vile mikono yangu haina kosa. Maana nimefuata njia za Yawe, wala sikujitenga na Mungu wangu kwa ajili ya uovu. Nimeshika maagizo yake yote, sikuacha kufuata masharti yake. Mbele yake nilikuwa mukamilifu, nimejikinga nisikuwe na kosa. Yawe amenilipa kwa kadiri ya haki yangu, kwa kadiri ya usafi wangu mbele yake. Wewe ni mwema kwa wema, mukamilifu kwa wakamilifu, bila kosa kwa wale ambao hawafanyi makosa, lakini mukali kwa waovu. Wewe unawaokoa wanyenyekevu, lakini unaangalia wenye majivuno kusudi uwashushe. Ee Yawe, wewe ni taa yangu. Yawe anafanya giza langu likuwe mwangaza. Kwa musaada wako, ninashinda kundi la waaskari; kwa musaada wa Mungu wangu, ninaruka kuta. Matendo ya Mungu ni makamilifu. Ahadi ya Yawe ni ya kuaminika. Yeye ni ngao kwa wote wanaomukimbilia. Nani anayekuwa Mungu isipokuwa Yawe? Nani anayekuwa kikingio isipokuwa Mungu wetu? Ni Mungu ambaye ananipatia nguvu, na anaifanya salama njia yangu. Ameiimarisha miguu yangu kama ya swala, na kunilinda salama juu ya milima. Ananifundisha kupigana vita, mikono yangu iweze kuvuta upinde wa shaba. Umenipa ngao yako ya kuniokoa; umenifanikisha kwa wema wako. Umepanua njia yangu wala miguu yangu haikuteleza. Niliwafuata waadui zangu na kuwaangamiza; sikurudi nyuma mpaka wamemalizika. Niliwamaliza kabisa. Hawakuinuka tena; walianguka chini ya miguu yangu. Wewe ulinijalia nguvu ya kupigana vita; uliwaporomosha waadui chini yangu. Uliwakimbiza waadui zangu, na wale walionichukia niliwaangamiza. Walitafuta musaada, lakini hakukukuwa wa kuwasaidia; walimulilia Yawe, lakini hakuwajibu. Niliwatwanga, wakakuwa kama mavumbi, nikawaponda na kuwakanyaga kama matope katika barabara. Wewe uliniokoa na mashambulizi ya watu wangu, ukanichunga kuwa mutawala wa mataifa. Watu nisiowajua walinitumikia. Wageni walinifikia wakinyenyekea; waliposikia tu habari zangu, walinitii. Wageni walivunjika moyo; wakakuja kutoka makimbilio yao wakitetemeka. Yawe anaishi! Asifiwe yeye kikingio changu! Atukuzwe Mungu, kikingio na mwokozi wangu. Yeye ameniwezesha kulipiza kisasi, ameweka mataifa chini yangu. Ameniokoa kutoka waadui zangu. Ee Yawe, ulinitukuza juu ya wapinzani wangu na kuniponyesha kutoka watesaji wakali. Kwa hiyo, nitakutukuza kati ya mataifa; nitaliimbia sifa jina lako. Mungu anamujalia mufalme wake ushindi mukubwa; anamutendea mema muchaguliwa wake, ndiye Daudi na wazao wake milele. Haya ni maneno ya mwisho ya Daudi. Ni ujumbe wa Daudi mwana wa Yese, ujumbe wa mutu ambaye Mungu alimufanya akuwe mukubwa, muchaguliwa wa Mungu wa Yakobo, mwimbaji muzuri wa zaburi wa Israeli: Roho wa Yawe amesema kwa njia yangu, aliyaweka maneno yake katika kinywa changu. Mungu wa Israeli amesema, Yeye Jiwe la Kufichamia la Israeli ameniambia: Mutu anayetawala watu kwa haki, anayewatawala akimwogopa Mungu, yeye ni kama mwangaza wa asubui, jua linapochomoza asubui isiyokuwa na mawingu. Yeye ni kama mvua inayootesha majani juu ya udongo. Hivi ndivyo jamaa yangu inavyokuwa mbele ya Mungu. Maana amefanya nami agano la kudumu milele; agano kamili na lenye kuwa imara. Naye atanifanikisha katika mahitaji yangu yote. Lakini watu waovu wote ni kama miiba inayotupwa tu, maana haiwezi kukamatwa kwa mukono; kwa kuigusa, sherti kutumia chuma au mupini wa mukuki. Watu hao wataangamizwa kabisa kwa moto. Haya ni majina ya mashujaa Daudi aliokuwa nao: Yosebu-Basebeti, wa muji wa Takemoni ndiye aliyekuwa kiongozi wa wale watatu. Yeye alipigana kwa mukuki wake, akaua watu mia nane mara moja katika vita. Halafu aliyefuata kati ya wale mashujaa watatu alikuwa Eleazari mwana wa Dodayi, wa ukoo wa Muahoa. Siku moja, Eleazari alikuwa pamoja na Daudi walipowatukana Wafilistini waliokuwa wamekusanyika kwa kupigana vita. Waisraeli waliwakimbia Wafilistini. Lakini Eleazari alisimama imara na kupigana na Wafilistini mpaka mukono wake uliposhindwa kupindika, ukabaki umebania upanga wake. Siku hiyo, Yawe alijipatia ushindi mukubwa. Nyuma ya ushindi ule, Waisraeli walirudi pahali Eleazari alipokuwa na kuteka vitu kutoka kwa Wafilistini waliouawa. Shujaa wa tatu alikuwa Sama mwana wa Age, wa muji wa Harari. Wafilistini walikusanyika kule Lehi, pahali palipokuwa shamba la manjegere nyingi. Kule Waisraeli waliwakimbia Wafilistini. Lakini alisimama imara katikati ya shamba lile kwa kulikinga, naye akawaua Wafilistini. Kwa hiyo, Yawe akajipatia ushindi mukubwa. Kisha, mashujaa watatu kati ya wakubwa makumi tatu waliteremuka wakati wa mavuno, wakamufikia Daudi kwenye pango kule Adulamu. Wakati ule kundi la waaskari wa Wafilistini lilikuwa limepiga kambi katika bonde la Refaimu. Naye Daudi wakati ule alikuwa katika maficho, nalo kundi la Wafilistini lilikuwa katika muji Betelehemu. Daudi akasema kwa hamu kubwa: “Ni nani atakayeweza kunipa maji ya kunywa kutoka katika kisima cha Betelehemu, kinachokuwa karibu na mulango wa muji!” Wale mashujaa wake watatu walitoka, wakapenya katikati ya kambi ya kundi la waaskari wa Wafilistini, wakaenda na kuchota maji katika kisima cha Betelehemu, karibu na mulango wa muji, wakamuletea Daudi. Lakini Daudi alikataa kuyakunywa, na pahali pa kuyakunywa, akayamwanga chini kama vile sadaka kwa Yawe, akisema: “Sina haki hata kidogo ya kunywa maji haya, ee Yawe. Maji haya si ni kama damu ya wale walioyahatarisha maisha yao kwa kuyaleta?” Kwa hiyo, Daudi hakuyakunywa maji hayo. Hayo ndiyo mambo waliyotenda wale mashujaa watatu. Abisayi mwana wa Zeruya na ndugu ya Yoabu alikuwa mukubwa wa mashujaa makumi tatu. Yeye alipigana kwa mukuki wake na watu mia tatu, akawaua, akajipatia sifa pamoja na wale mashujaa watatu. Alikuwa na heshima zaidi kati ya wale mashujaa makumi tatu. Kwa hiyo akakuwa jemadari wao, lakini hakukuwa shujaa kama wale mashujaa watatu. Naye Benaya mwana wa Yehoyada wa muji Kabuseli, alikuwa askari shujaa ambaye alifanya mambo mengi ya ajabu. Aliwaua mashujaa wawili kutoka Moabu, na siku moja wakati wa teluji, alishuka katika shimo na kuua simba. Vilevile, aliua mutu mumoja jitu wa Misri. Mumisri yule alikuwa na mukuki, lakini Benaya alimwendea akiwa na fimbo tu, akamunyanganya mukuki ule, na kumwua Mumisri yule kwa mukuki wake mwenyewe. Benaya mwana wa Yehoyada alifanya mambo haya, akajipatia sifa pamoja na wale mashujaa watatu. Akakuwa na heshima pamoja na wale mashujaa makumi tatu, ingawa hakukuwa kama wale mashujaa watatu. Na Daudi akamupa cheo cha mukubwa wa waaskari walinzi wake. Asaeli ndugu ya Yoabu, alikuwa mumoja wa mashujaa makumi tatu. Mashujaa wengine wa Daudi walikuwa: Elihanani, mwana wa Dodo wa Betelehemu; Sama na Elika, wote wa muji Harodi; Helesi wa muji Palti; Ira mwana wa Ikesi wa muji Tekoa; Abiezeri wa muji Anatoti; Mebunayi wa muji Husa: Zalmoni wa muji Ahoa; Maharai wa muji Netofa; Helebu mwana wa Bana wa muji Netofa; Itayi mwana wa Ribayi toka Gibea katika kabila la Benjamina; Benaya wa muji Piratoni; Hidayi wa vijito vya Gasi; Abialboni wa muji Araba; Azimaweti wa muji Bahurimu; Eliabu wa muji Salaboni; wana wa Yaseni; Yonatani; na Sama wa muji Harari; Ahiamu mwana wa Sarari wa muji Arari; Elifeleti mwana wa Ahasibayi wa Maka; Eliamu mwana wa Ahitofeli wa Gilo; Hesiro wa muji Karmeli: Parayi wa muji Araba; Igali mwana wa Natani wa inchi ya Zoba; Bani wa muji Gadi; Zeleki wa inchi ya Waamoni; Naharayi wa muji Beroti aliyekuwa mubebaji wa silaha wa Yoabu mwana wa Zeruya; Ira na Garebu wa ukoo wa Yeteri; na Uria wa inchi ya Wahiti. Wote pamoja walikuwa mashujaa makumi tatu na saba. Kwa mara nyingine, Yawe aliwakasirikia Waisraeli, akamusukuma Daudi kuwatendea vibaya, akamwambia awahesabu watu wa Israeli na watu wa Yuda. Halafu, mufalme akamwambia Yoabu na majemadari wa kundi la waaskari waliokuwa pamoja naye: “Muzunguke katika makabila yote ya Waisraeli kutokea Dani mpaka Beri-Seba, muwahesabu watu kusudi nipate kujua jumla yao.” Lakini Yoabu akamwambia mufalme: “Yawe, Mungu wako, awaongeze Waisraeli mara mia kuliko walivyokuwa sasa, nawe bwana wangu mufalme upate kuona ongezeko hilo kwa macho yako mwenyewe. Lakini, kwa nini wewe bwana wangu mufalme unapendezwa na jambo hili?” Lakini neno la mufalme lilikuwa na nguvu zaidi mbele ya Yoabu na majemadari wa kundi la waaskari. Basi, Yoabu na majemadari wa waaskari wakaondoka mbele ya mufalme, wakaenda kuwahesabu Waisraeli. Walivuka muto Yordani wakianzia kuhesabu watu tangu Aroeri na muto unaokuwa katika bonde kuelekea Gadi mpaka Yazeri. Kisha, wakaenda Gileadi halafu Kadesi katika inchi ya Wahiti, halafu wakafika Dani na kutoka Dani wakazunguka kwenda Sidona, na kufika kwenye ukuta wa muji wa Tiro, wakaingia kwenye miji yote ya Wahivi na ya Wakanana. Kisha, walitoka wakaenda Negebu ya Yuda kule Beri-Seba. Walipokwisha kupita katika inchi yote, walirudia Yerusalema nyuma ya miezi kenda na siku makumi mbili. Halafu Yoabu alimupelekea mufalme jumla ya watu. Katika inchi ya Israeli kulikuwa wanaume mashujaa elfu mia ine wenye ujuzi wa kutumia mapanga; na katika Yuda, kulikuwa wanaume elfu mia tano. Lakini Daudi alisumbuliwa sana katika roho yake kisha kuwahesabu watu. Kwa hiyo, Daudi akamwambia Yawe: “Nimetenda zambi kubwa kwa tendo nililolifanya. Lakini sasa, ee Yawe, ninakusihi unisamehe mimi mutumishi wako, maana nimefanya jambo la kipumbafu kabisa.” Daudi alipoamuka kesho yake asubui, neno la Yawe lilimufikia nabii Gadi, mwonaji wa mufalme Daudi, kusema hivi: “Kwenda umwambie Daudi hivi: ‘Yawe anasema hivi: Ninakupa mambo matatu, nawe ujichagulie moja kati yao, nami nitakutendea nalo.’ ” Halafu, Gadi akamwendea Daudi na kumwelezea, akisema: “Unapendelea njaa ya miaka saba ikuje katika inchi yako? Au wewe uwakimbie waadui zako kwa miezi mitatu wanapokufuatilia? Au kuwe siku tatu ambapo inchi yako itakuwa na ugonjwa mukali? Fikiri unipe jibu nitakalomupa yeye aliyenituma.” Daudi akamujibu Gadi: “Nina mashaka makubwa! Lakini afazali kuazibiwa na Yawe, kuliko kutiwa katika mikono ya watu, maana yeye ana rehema sana.” Basi, Yawe akawaletea Waisraeli ugonjwa, tangu asubui mpaka wakati uliopangwa. Watu elfu makumi saba walikufa katika inchi yote kutoka Dani mpaka Beri-Seba. Lakini wakati malaika aliponyoosha mukono wake kuelekea Yerusalema kwa kuuangamiza, Yawe alibadilisha nia yake. Yawe akamwambia yule malaika aliyetimiza maangamizi kwa watu: “Basi! Inatosha; rudisha mukono wako.” Malaika wa Yawe alikuwa amesimama karibu na kiwanja cha kupepetea ngano cha Arauna wa muji wa Yebusi. Daudi alipomwona yule malaika aliyekuwa anawaua watu, alimwambia, Yawe: “Mimi ndiye ninayekuwa na kosa! Mimi mwenyewe nimekosa! Hawa watu wapole hawakufanya uovu. Ninakusihi sana uniazibu mimi na jamaa ya baba yangu.” Siku hiyo hiyo Gadi akamwendea Daudi, akamwambia: “Panda juu, umujengee Yawe mazabahu, katika kiwanja cha kupepetea ngano cha Arauna wa muji wa Yebusi.” Basi, Daudi akapanda juu kufuatana na neno la Gadi kama Yawe alivyomwamuru. Arauna alipoangalia upande wa chini alimwona mufalme akimusogelea pamoja na watumishi wake, naye akatoka, akaenda na kuinama uso mpaka chini mbele ya mufalme. Kisha Arauna akamwuliza mufalme: “Kwa nini bwana wangu mufalme amenifikia mimi mutumishi wake?” Daudi akamujibu: “Nimekuja kununua kiwanja chako cha kupepetea ngano kusudi nimujengee Yawe mazabahu kusudi ugonjwa mukali uliowapata watu ukome.” Naye Arauna akamwambia Daudi: “Bwana wangu mufalme, utwae chochote unachoona kinafaa na utolee sadaka. Mimi ninawatoa ngombe dume hawa kwa ajili ya sadaka ya kuteketezwa na vifaa hivi vya kupepetea na nira za ngombe kuwa kuni. Ninakupa hivi vyote, ee mufalme. Ninatumaini Yawe, Mungu wako, atapokea sadaka yako kwa wema.” Lakini mufalme akamwambia Arauna: “Hapana! Wewe hautanipa kitu chochote. Mimi nitavinunua kwako kwa bei yake. Sitamutolea Yawe, Mungu wangu, sadaka za kuteketezwa ambazo sikununua.” Hivyo, mufalme Daudi alinunua kiwanja cha kupepetea na ngombe dume kwa bei ya vikoroti makumi tano vya feza. Kisha Daudi akamujengea Yawe mazabahu pahali pale na kumutolea sadaka za kuteketezwa na za amani. Basi, Yawe akayakubali maombi kwa ajili ya inchi, na ule ugonjwa mukali uliowapata Waisraeli ikakoma. Wakati mufalme Daudi alipokuwa muzee sana, watumishi wake walimufunika kwa mablanketi, lakini, hata hivyo, hakuweza kupata joto. Kwa hivyo, wakamwambia: “Bwana wetu mufalme, afazali tukutafutie binti akutumikie na kukutunza; alale pamoja nawe kusudi akupatie joto.” Basi, wakatafutatafuta binti muzuri katika inchi yote ya Israeli. Kukapatikana binti mumoja muzuri anayeitwa Abisagi Musunami. Wakamuleta kwa mufalme. Binti yule, alikuwa muzuri sana. Basi, akaanza kumutumikia na kumutunza mufalme, lakini mufalme hakumujua kimwili. Wakati ule, Adonia mwana wa Daudi kutoka muke wake Hagiti, akaanza kujivuna kwamba yeye ndiye atakayekuwa mufalme. Basi, akajitayarishia magari, wapanda-farasi na watu makumi tano wa kumutangulia. Lakini baba yake Daudi hakukuwa amemukaripia mwana wake hata mara moja wala kumwuliza kwa nini alikuwa amefanya hivyo. Adonia alikuwa mwenye sura ya kupendeza sana na alikuwa amemufuata Abusaloma kwa kuzaliwa. Adonia akafanya shauri na Yoabu mwana wa Zeruya, na kuhani Abiatari. Nao wakamufuata na kumwunga mukono. Lakini kuhani Zadoki, Benaya mwana wa Yehoyada, nabii Natani na Simei, na Rei pamoja na walinzi wa Daudi, hawakumwunga Adonia mukono. Siku moja, Adonia alitoa sadaka ya kondoo, ngombe na wana-ngombe wanono kwenye Jiwe la Zoheleti, karibu na chemichemi inayoitwa Enrogeli. Akawaalika kwenye karamu ya sadaka hiyo wandugu zake wote, ni kusema wana wengine wa mufalme, na watumishi wote wa mufalme wanaokuwa wa kabila la Yuda. Lakini hakuwaalika nabii Natani, Benaya, walinzi wa mufalme na ndugu yake Solomono. Kisha, Natani akamwendea Batiseba mama ya Solomono, akamwuliza: “Haujasikia kwamba Adonia mwana wa Hagiti amejiweka kuwa mufalme na bwana wetu Daudi hana habari? Basi, kama ukitaka kuyaokoa maisha yako na ya mwana wako Solomono, ninakushauria hivi: Umwendee mufalme Daudi, umwulize: ‘Bwana wangu mufalme, si uliniapia mimi mujakazi wako ukisema: Mwana wako Solomono atatawala nyuma yangu, na ataikaa juu ya kiti changu cha kifalme? Imekuwa namna gani basi, sasa Adonia anatawala?’ Na utakapokuwa ungali unaongea na mufalme, mimi nitaingia na kuyahakikisha maneno yako.” Basi, Batiseba alimwendea mufalme ndani ya chumba chake. Wakati ule, mufalme alikuwa muzee sana, naye Abisagi Musunami alikuwa akimuchunga. Batiseba aliinama kwa heshima mbele ya mufalme, naye mufalme akamwuliza: “Unataka nini?” Batiseba akamujibu: “Bwana wangu, uliniapia mimi mujakazi wako mbele ya Mungu wako Yawe, ukisema: ‘Mwana wako Solomono atatawala nyuma yangu, na ataikaa juu ya kiti changu cha kifalme.’ Lakini, sasa, Adonia anatawala ingawa wewe bwana wangu mufalme haujui juu ya hayo. Ametoa sadaka ya ngombe, ya wana-ngombe wanono, na kondoo wengi, na amewaalika wana wote wa mufalme, kuhani Abiatari, na Yoabu jemadari wa makundi yako ya waaskari, lakini mutumishi wako Solomono hakualikwa. Na sasa, bwana wangu mufalme, Waisraeli wote wanakungojea, kusudi uwaambie yule atakayeikaa juu ya kiti chako nyuma yako, bwana wangu mufalme. Na kama sivyo, itatokea kwamba, wakati wewe bwana wangu mufalme utakapokufa, mimi pamoja na mwana wangu Solomono tutahesabiwa kama wenye kosa.” Wakati Batiseba alipokuwa akizungumuza na mufalme, nabii Natani aliingia katika nyumba ya kifalme. Nao watu wakamwambia mufalme: “Nabii Natani yuko hapa.” Naye alipomufikia mufalme, aliinama mbele ya mufalme mpaka uso ukafika chini kwenye udongo. Halafu Natani akasema: “Bwana wangu mufalme, ni kweli kwamba ulisema hivi: ‘Adonia atatawala nyuma yangu, na ataikaa juu ya kiti changu cha kifalme’? Kwa maana leo alienda kutoa sadaka ya ngombe, wana-ngombe wanono na kondoo wengi na amewaalika wana wote wa mufalme, Yoabu jemadari wa waaskari, na kuhani Abiatari, na sasa wanakula na kunywa mbele yake, na kusema: ‘Mufalme Adonia aishi!’ Lakini hakunialika mimi mutumishi wako wala kuhani Zadoki wala Benaya mwana wa Yehoyada wala mutumishi wako Solomono. Mbona yote hayo umeyafanya wewe bwana wangu mufalme, bila kuwaambia watumishi wako mutu atakayeikaa juu ya kiti chako cha kifalme nyuma yako?” Naye mufalme Daudi akajibu: “Uniitie Batiseba.” Batiseba alimwendea mufalme na kusimama mbele yake. Halafu mufalme aliapa, akisema: “Kama vile Yawe anavyoishi, yule aliyekomboa roho yangu katika taabu nyingi, kama nilivyokuapia mbele ya Yawe, Mungu wa Israeli, nikisema: ‘Mwana wako Solomono atatawala nyuma yangu, na ataikaa juu ya kiti changu cha kifalme pahali pangu’, ndivyo nitakavyofanya leo.” Batiseba akainama uso mpaka chini, kwa heshima mbele ya mufalme, na kusema: “Bwana wangu mufalme Daudi aishi milele!” Kisha mufalme Daudi akasema: “Uniitie kuhani Zadoki, nabii Natani na Benaya mwana wa Yehoyada.” Nao wakafika kwa mufalme. Naye mufalme akawaambia: “Kwenda na watumishi wangu mimi bwana wako, umupandishe mwana wangu Solomono juu ya nyumbu wangu, umupeleke kule Gihoni. Halafu umuruhusu kuhani Zadoki na nabii Natani wamupakae mafuta akuwe mufalme wa Israeli. Kisha mupige baragumu na kusema: ‘Mufalme Solomono aishi!’ Nanyi mutamufuata, naye atakuja na kuikaa juu ya kiti changu cha kifalme kwa pahali pangu; nami nimemuchagua kuwa mutawala juu ya Israeli na juu ya Yuda.” Benaya mwana wa Yehoyada akamujibu mufalme: “Amina! Yawe, Mungu wa bwana wangu mufalme, aseme vile vile. Kama Yawe alivyokuwa pamoja na bwana wangu mufalme, akuwe vilevile na Solomono, na akitukuze kiti chake cha kifalme kuliko kiti cha kifalme cha bwana wangu mufalme Daudi.” Basi, kuhani Zadoki, nabii Natani na Benaya mwana wa Yehoyada, na Wakereti na Wapeleti, wote walishuka, wakamupandisha Solomono kwenye nyumbu wa mufalme Daudi, na kumupeleka mpaka Gihoni. Kisha kuhani Zadoki alitwaa pembe za mafuta kutoka katika hema na kumupakaa Solomono mafuta kuwa mufalme. Kisha walipiga baragumu na watu wote wakasema: “Mufalme Solomono aishi!” Halafu watu wote walimufuata, wakipiga mazomari, wakafurahi kwa shangwe kubwa, hata inchi ikatikisika kwa sauti zao. Basi, Adonia pamoja na waalikwa waliokuwa naye walikuwa wakimaliza sherehe. Naye Yoabu aliposikia sauti ya baragumu, alisema: “Makelele hayo katika muji ni ya nini?” Alipokuwa akisema, Yonatani mwana wa kuhani Abiatari akaingia. Adonia akasema: “Karibu, maana wewe ni mutu hodari na unaleta habari nzuri.” Yonatani akamujibu Adonia: “Hapana. Mufalme Daudi amemusimika Solomono kuwa mufalme. Naye mufalme amemupeleka pamoja na kuhani Zadoki, nabii Natani, Benaya mwana wa Yehoyada, na Wakereti na Wapeleti, nao wamemupandisha juu ya nyumbu wa mufalme. Kisha kuhani Zadoki na nabii Natani wakamupakaa mafuta akuwe mufalme kule Gihoni. Halafu wametoka hapo wakifurahi, ndiyo sababu ya makelele hayo unayosikia. Sasa Solomono anaikaa juu ya kiti cha kifalme. Zaidi ya hayo, watumishi wa mufalme walikuja kumupa pole bwana wetu mufalme Daudi wakisema: ‘Mungu wako alifanye jina la Solomono kuwa lenye sifa kuliko lako; tena akitukuze kiti chake cha kifalme kuliko kiti chako.’ Halafu mufalme akainama juu ya kitanda na kuomba akisema: ‘Asifiwe Yawe, Mungu wa Israeli, ambaye amemufanya muzao wangu kuwa mufalme kwa pahali pangu, na ambaye amenipa maisha hata nimeyaona mambo hayo.’ ” Basi, waalikwa wa Adonia wakaogopa sana, wakaondoka na kutawanyika. Naye Adonia, kwa sababu alimwogopa Solomono, akakimbilia katika hema la Yawe, akazishika pembe za mazabahu apate kuponyoka. Mufalme Solomono akapata habari kwamba Adonia alikuwa amekimbilia ndani ya hema, na kwamba anashikilia pembe za mazabahu akisema: “Sitaondoka hapa mpaka mufalme Solomono atakaponihakikishia kwamba hataamuru niuawe.” Mufalme Solomono akasema: “Nikimwona kuwa mwaminifu basi, hatapata hasara yoyote. Lakini nikimwona kuwa mwovu, hakika atakufa.” Basi, mufalme Solomono akaagiza Adonia aitwe kutoka katika hema, akuje kwake. Adonia akafika mbele ya mufalme, akainama kwa heshima. Mufalme akamwambia: “Kwenda kwa nyumba yako.” Daudi alipokaribia kufa, alimwita mwana wake Solomono, akamupa maagizo akisema: “Mwana wangu, kama inavyokuwa kawaida kwa viumbe vyote kufa, siku zangu zimekwisha. Ukuwe imara na hodari. Timiza maagizo ya Yawe, Mungu wako, ufuate njia zake na kushika masharti yake, amri zake, maagizo yake na maamuzi yake kama ilivyoandikwa katika Sheria ya Musa. Kwa hiyo, utafanikiwa katika kila jambo unalofanya na kokote unakoenda. Naye Yawe atatimiza ahadi yake aliyotoa aliponiambia kwamba, ikiwa wazao wangu watatii amri zake na kumutumikia kwa uaminifu na kwa moyo wote, hakutakosekana mumoja wao kwa kutawala Israeli nyakati zote. “Zaidi ya hayo, unajua vilevile yale Yoabu mwana wa Zeruya aliyonitendea, jinsi alivyowatendea majemadari wawili wa waaskari wa Israeli, Abeneri mwana wa Neri, na Amasa mwana wa Yeteri. Aliwaua wakati wa amani akitaka kulipiza kisasi kwa mauaji waliyofanya wakati wa vita. Aliwaua watu wasiokuwa na kosa, nami nikabeba lazima ya kifo cha watu wale kwa ajili ya vitendo vyake. Basi, wewe fanya kadiri ya hekima yako, lakini tu usimwache akufe kwa amani. “Lakini uwatendee mema wana wa Barzilayi, yule Mugileadi, wakuwe kati ya wale wanaokula kwenye meza yako, kwa sababu walinitendea mema wakati nilipomukimbia ndugu yako Abusaloma. Vilevile, kuko Simei mwana wa Gera, wa kabila la Benjamina wa muji wa Bahurimu, ambaye aliniapiza na kunilaani vikali nilipokwenda kule Mahanaimu; lakini alipokuja kunipokea kwenye muto Yordani, nilimwapia kwa jina la Yawe nikimwambia: ‘Sitakuua kwa upanga.’ Lakini wewe usimwache bila kumwazibu. Una hekima, utajua utakalomufanyia. Ingawa yeye ana imvi, usimwache. Umwue ingawa ni muzee.” Daudi akakufa na kuzikwa katika muji wake. Alikuwa ametawala inchi ya Israeli kwa muda wa miaka makumi ine; miaka saba akiwa Hebroni, na miaka makumi tatu na mitatu akiwa Yerusalema. Basi, Solomono akaikaa katika kiti cha kifalme kwa pahali pa baba yake Daudi, na ufalme wake ukaimarika. Nyuma, Adonia mwana wa Hagiti, alimwendea Batiseba, mama ya Solomono. Batiseba akamwuliza: “Unaleta habari ya amani?” Adonia akamujibu: “Ndiyo, ninaleta habari ya amani. Lakini, nina jambo moja tu la kukuambia.” Batiseba akamwambia: “Sema tu.” Adonia akamwambia: “Unajua kwamba ni mimi ndiye ningalikuwa mufalme, na hata Israeli yote ilikuwa inanitazamia nikuwe mufalme. Lakini, mambo yakageuka na ndugu yangu akanipindua, kwa sababu hayo ndiyo yaliyokuwa mapenzi ya Yawe. Sasa, nina ombi moja tu ambalo ninakusihi usinikatalie.” Batiseba akamwambia: “Sema tu.” Naye akasema: “Tafazali, ninakusihi umwombe mufalme Solomono aniruhusu nimukamate Abisagi, yule Musunami, akuwe muke wangu, kwa maana ninajua hatakukatalia wewe.” Batiseba akamwambia: “Sawa; nitazungumuza na mufalme kwa jina lako.” Basi, Batiseba akamwendea mufalme Solomono kwa kumwelezea ombi la Adonia. Mufalme akasimama kwenda kumupokea mama yake, akainama mbele yake. Halafu, akaikaa katika kiti chake cha kifalme, akaagiza mama yake aletewe kiti, naye akaikaa kwa upande wa kuume wa mufalme. Batiseba akasema: “Nina ombi dogo tafazali ulikubali, na ninakuomba usinikatalie.” Mufalme akamwambia: “Sema ombi lako mama yangu, kwa sababu sitakukatalia.” Naye akasema: “Umuruhusu ndugu yako Adonia amwoe Abisagi, yule Musunami.” Mufalme Solomono akamwuliza mama yake: “Kwa nini unataka nimupe Abisagi? Hii ni sawa kabisa na kumutakia ufalme wangu! Kumbuka kwamba yeye ni mukubwa yangu, na si ile tu, kuhani Abiatari na jemadari Yoabu mwana wa Zeruya, wako upande wake!” Hapo mufalme Solomono akaapa kwa jina la Yawe, akisema: “Mungu aniue ikiwa Adonia hatakufa kwa sababu ya kutoa ombi hili! Sasa basi, kama vile Yawe anavyoishi, yule aliyeniweka na kuniimarisha katika ufalme wa baba yangu Daudi na kutimiza ahadi yake ya kunipa kiti cha kifalme mimi na wazao wangu, Adonia atakufa leo!” Halafu mufalme Solomono akatoa amri kwa Benaya mwana wa Yehoyada; naye akamwendea Adonia, akamwua. Mufalme Solomono akamwambia kuhani Abiatari: “Ondoka uende katika shamba lako, kule Anatoti. Unastahili kufa wewe. Lakini sasa, sitakuua kwa sababu ulilishugulikia Sanduku la Agano la Yawe ulipokuwa na baba yangu Daudi, ukateswa pamoja naye.” Basi, mufalme Solomono akamufukuza Abiatari, asikuwe kuhani wa Yawe. Hivyo likatimia neno alilosema Yawe kule Shilo, juu ya Eli na ukoo wake. Yoabu alipopata habari, alikimbilia katika hema ya Mungu na kushikilia pembe za mazabahu kwa maana alikuwa amemwunga Adonia mukono ingawa mbele hakukuwa na Abusaloma. Mufalme Solomono aliposikia kwamba Yoabu yuko katika hema la Mungu na kwamba amesimama kwenye mazabahu, alimutuma Benaya mwana wa Yehoyada, akisema: “Kwenda umupige.” Basi, Benaya akaenda katika hema la Mungu, akamwambia Yoabu: “Mufalme ameamuru utoke inje.” Yoabu akajibu: “Mimi sitatoka; nitakufia hapahapa.” Benaya akarudi kwa mufalme na kumwelezea jinsi Yoabu alivyojibu. Solomono akasema: “Fanya sawa alivyosema. Umwue na kumuzika. Hivyo, mimi na wazao wengine wote wa Daudi hatutabeba lazima ya vitendo vya Yoabu vya kuwaua watu wasiokuwa na kosa. Mungu atamwazibu Yoabu kwa mauaji hayo aliyoyafanya bila baba yangu kuwa na habari. Yeye aliwaua watu wawili ambao walikuwa wa maana zaidi kuliko yeye, tena walimupita kwa wema; aliwaua Abeneri mwana wa Neri, jemadari wa kundi la waaskari Waisraeli, na Amasa mwana wa Yeteri, jemadari wa waaskari wa Yuda. Azabu ya mauaji hayo itakuwa juu ya Yoabu na wazao wake milele. Lakini Yawe atawabariki siku zote Daudi na wazao wake watakaoikalia kiti chake cha kifalme.” Basi, Benaya mwana wa Yehoyada akaenda katika hema, akamwua Yoabu ambaye alizikwa katika shamba lake, katika mbuga. Mufalme akamuweka Benaya mwana wa Yehoyada kuwa jemadari wa kundi la waaskari kwa pahali pa Yoabu, na Zadoki akakuwa kuhani pahali pa Abiatari. Halafu mufalme akaagiza Simei aitwe, akamwambia: “Ujijengee nyumba humu Yerusalema, ukae hapa bila kwenda pahali pengine popote. Maana siku utakapotoka na kuvuka kijito Kidroni, ninakuambia kweli utakufa na kubeba lazima ya kifo chako wewe mwenyewe.” Simei akajibu: “Ni vizuri, mufalme. Nitafanya kama ulivyosema.” Basi, akakaa Yerusalema kwa muda murefu. Lakini kwa mwisho wa mwaka wa tatu, watumwa wawili wa Simei walitoroka, wakaenda kwa Akisi mwana wa Maka, mufalme wa Gati. Habari zilipomufikia kwamba wako Gati, Simei alipanda juu ya punda wake, akaenda kule kwa kuwatafuta, kwa mufalme Akisi. Basi, akafika, akawapata, akawarudisha kwake. Mufalme Solomono alipopata habari kwamba Simei alikuwa ametoka Yerusalema, akaenda Gati na kurudi, alimwita Simei na kumwambia: “Si wewe ndiwe uliniapia kwa jina la Yawe kwamba hautatoka Yerusalema? Nami si nilikuonya kwamba hakika utakufa kama ukisubutu kwenda inje? Nawe ulikubali, ukaniambia: ‘Ni vizuri, nitatii’. Mbona basi, umevunja kiapo chako kwa Yawe na kutojali amri niliyokupa?” Mufalme aliendelea kumwambia Simei: “Unayajua wazi maovu uliyomutendea baba yangu Daudi. Sasa, kwa sababu ya hayo, Yawe atakuazibu. Lakini mimi atanibariki, na kiti cha kifalme cha Daudi kitaimarishwa mbele ya Yawe milele.” Hapo, mufalme akamwamuru Benaya mwana wa Yehoyada, naye akatoka, akamupiga na kumwua Simei. Basi, ufalme ukaimarika chini ya Solomono. Solomono alifanya mapatano na mufalme wa Misri, kwa kumwoa binti yake. Akamuleta binti wa mufalme wa Misri na kumuweka katika muji wa Daudi, mpaka alipomaliza kujenga nyumba yake mwenyewe, nyumba ya Yawe, na ukuta wa kuuzunguka Yerusalema. Kwa wakati ule, watu walikuwa wakitoa sadaka kule juu ya vilima, kwa kuwa nyumba ya Mungu ilikuwa bado haijajengwa. Solomono alimupenda Yawe, akashika masharti ya baba yake Daudi; lakini tu, naye alitoa sadaka na kufukiza ubani juu ya vilima. Wakati mumoja, Solomono alikwenda kutoa sadaka kule kwenye kilima cha Gibeoni, maana palikuwa ndipo pahali pakubwa pa ibada. Ilikuwa ni kawaida ya Solomono kutoa maelfu ya sadaka za kuteketezwa katika mazabahu hiyo. Kule Gibeoni, Yawe alimutokea Solomono katika ndoto usiku, akamwambia: “Omba kitu chochote unachotaka nami nitakupa.” Solomono akamwambia: “Ulimwonyesha wema mwingi mutumishi wako Daudi, baba yangu, kwa sababu alikutumikia kwa uaminifu, kwa haki na kwa moyo wa usawa; na umedumisha mema yako kwa kumupa mwana anayeikaa sasa kwenye kiti chake cha kifalme. Ee Yawe, Mungu wangu, umeniweka mimi mutumishi wako kuwa mufalme pahali pa baba yangu Daudi, ijapokuwa ningali mutoto mudogo na sijui namna ya kutimiza kazi hii. Na hapa umeniweka kati ya watu wako ambao umewachagua; nao ni wengi hata hawawezi kuhesabika kwa sababu ya wingi wao. Kwa hiyo, ninakuomba unipe mimi mutumishi wako moyo wa hekima nipate kuamua watu wako, niweze kutambua mazuri na mabaya; maana ni nani anayeweza kuhukumu watu wako wanaokuwa wengi hivi?” Ombi hili la Solomono lilimufurahisha Yawe, naye akamwambia: “Kwa sababu umetoa ombi hili, na haukujiombea maisha marefu au mali, na wala haukuomba waadui zako waangamizwe, lakini umejiombea hekima ya kutoa hukumu au kutenda haki, basi, sasa ninakutimizia kama ulivyoomba. Ninakupa hekima na akili kwa kipimo ambacho hakuna mutu mwingine aliyepata kuwa nacho mbele yako, na wala hakutatokea mwingine kama wewe nyuma yako. Vilevile, nitakupa yale ambayo haukuomba: nitakupa utajiri na heshima zaidi ya mufalme mwingine yeyote wa nyakati zako. Tena kama ukifuata njia yangu na kushika masharti na amri zangu kama vile baba yako Daudi alivyofanya, basi, nitakupa maisha marefu.” Solomono alipoamuka, alitambua kwamba ilikuwa ndoto. Halafu akarudi Yerusalema, akasimama mbele ya Sanduku la Agano la Yawe, akamutolea sadaka za kuteketezwa na za amani. Halafu akawafanyia watumishi wake wote karamu. Siku moja, wanawake wawili wakahaba walikwenda kwa mufalme Solomono. Mumoja wao akasema: “Ee bwana wangu, mimi na huyu mwenzangu tunakaa nyumba moja. Mimi nilizaa mutoto mwanaume huyu akiwa pale. Nyuma ya siku tatu huyu naye akazaa mutoto mwanaume. Hakukukuwa mutu mwingine ndani ya nyumba isipokuwa sisi wawili tu. Halafu, usiku mumoja, mutoto wake akakufa kwa sababu alimulalia. Kisha akaamuka usiku kati, akamutwaa mwana wangu kutoka kwangu wakati mimi niko katika usingizi, akamulalisha kwenye kufua chake. Halafu akatwaa maiti ya mwana wake, akailalisha kwenye kifua changu. Nilipoamuka asubui na kutaka kumunyonyesha mwana wangu, nikakuta mutoto amekufa. Nilipochunguza sana, nikagundua kwamba hakukuwa mwana wangu niliyemuzaa.” Lakini yule mwanamuke mwingine akasema: “Hapana! Wa kwangu ndiye anayekuwa muzima na wa kwako ndiye aliyekufa”. Naye mwanamuke wa kwanza akasema: “Hapana! Mutoto wako ndiye aliyekufa, wangu ni huyo anayekuwa muzima!” Basi, wakaendelea kubishana hivyo mbele ya mufalme. Halafu mufalme Solomono akasema: “Kila mumoja wenu anadai kwamba mutoto wake ndiye mwenye kuwa muzima na kwamba aliyekufa si wake.” Basi, mufalme akaagiza: “Muniletee upanga!” Wakamuletea mufalme upanga. Mufalme akasema: “Mukate huyo mutoto muzima vipande viwili, uwape wamama hawa kila mumoja nusu ya mutoto.” Yule mwanamuke aliyekuwa mama ya huyo mutoto anayekuwa muzima alishikwa na huruma juu ya mwana wake, akamwambia mufalme: “Tafazali mufalme, musimwue mutoto. Mumupe mwenzangu huyo mutoto mwenye kuwa muzima, amutwae yeye.” Lakini yule mwanamuke mwingine akasema: “Hapana! Mutoto asikuwe wangu wala wake. Mumukate vipande viwili.” Mufalme Solomono akasema: “Usimwue mutoto! Umupe mwanamuke wa kwanza amutwae, maana yeye ndiye mama yake.” Watu wote wa Israeli waliposikia juu ya hukumu ya mufalme, walimwogopa. Wakatambua kwamba alikuwa na hekima ya Mungu iliyomuwezesha kutoa hukumu za haki. Solomono alichagua maliwali kumi na wawili kwa inchi nzima ya Israeli. Hao walipewa kazi ya kutafuta chakula kwa ajili ya mufalme na nyumba yake. Kila mumoja wao alileta chakula kutoka jimbo lake kwa mwezi mumoja kila mwaka. Watu wa Yuda na wa Israeli walikuwa wengi kama muchanga wa bahari, nao walikuwa wakikula, wakikunywa, na kufurahi. Solomono alitawala falme zote kuanzia kwa muto Furati mpaka katika inchi ya Wafilistini, na kuendelea hata kwa mupaka na Misri. Mataifa yote yalimutumikia na kulipa kodi kwake wakati wote wa maisha yake. Chakula Solomono alichohitaji kwa siku moja kwa ajili ya nyumba yake kilikuwa unga laini madebe mia tatu na makumi sita, na unga wa kawaida madebe mia saba na makumi mbili, ngombe wanono kumi, na ngombe makumi mbili toka shamba la malisho, kondoo mia moja pamoja na kulungu, paa, swala na kuku wanono. Inchi yote upande wa magaribi wa muto Furati, kutokea Tifusa mpaka muji wa Gaza, ilikuwa chini ya utawala wake. Wafalme wote upande wa magaribi wa muto Furati walikuwa chini yake, na alikuwa na amani na inchi zote jirani. Siku zote za utawala wake, watu wa Yuda na wa Israeli walikaa salama, kila mutu akistawi kwenye miti yake ya mizabibu na ya tini. Solomono alikuwa na vibanda elfu makumi ine kwa ajili ya farasi wa magari yake ya kukokotwa, na waaskari wapanda-farasi elfu kumi na mbili. Wale maliwali wake kumi na wawili, kila mumoja kwa mwezi aliopangiwa, walipeleka chakula cha kutosha kwa ajili ya mufalme na wale wote waliokula katika nyumba yake. Mahitaji yao yote yalitoshelezwa. Zamu ya kila mumoja ilipofika, alipeleka vilevile shayiri na majani ya kulisha farasi na nyama wanaokimbia mbio. Mungu alimupa Solomono hekima zaidi na akili kwa wingi. Maarifa yake yalikuwa kama muchanga wa bahari, hayakukuwa na kipimo. Hekima ya Solomono iliipita hekima ya watu wa mashariki na iliishinda hekima ya watu wa Misri. Aliwashinda watu wote kwa hekima; aliwashinda Etani, yule Muezra, Hemani na Kalkoli na Darda, wana wa Maholi; na sifa zake zilienea katika mataifa yote jirani. Alitunga mezali elfu tatu na nyimbo elfu moja na tano. Alizungumuzia habari za miti, kuanzia mwerezi unaokuwa Lebanoni, hata hisopo, muti unaotambaa juu ya ukuta. Alizungumuzia vilevile juu ya nyama, ndege, viumbe vinavyotambaa, na samaki. Watu kutoka mataifa yote, na wafalme wote waliopata kusikia habari juu ya hekima yake, walikuja kumusikiliza. Mufalme Hiramu wa Tiro, aliyekuwa rafiki ya Daudi, alipopata habari kwamba Solomono amekuwa mufalme pahali pa baba yake, alituma watumishi kwake. Halafu Solomono akamupelekea Hiramu ujumbe huu: “Unajua kwamba baba yangu Daudi hakuweza kumujengea Yawe, Mungu wake, hekalu la kumwabudia, kwa sababu ya vita vilivyomuzunguka pande zote mpaka hapo Yawe alipomupatia ushindi. Lakini sasa, Yawe, Mungu wangu, amenijalia amani pande zote. Sina adui wala taabu. Basi, nimeamua kumujengea Yawe, Mungu wangu, nyumba ya kumwabudia. Na hii ni sawa kabisa kama Yawe alivyomwahidi baba yangu akisema: ‘Mwana wako ambaye nitamwikalisha katika kiti chako cha kifalme, atanijengea nyumba.’ Sasa basi, uwaamuru watu wako wanikatie miti ya mierezi ya Lebanoni. Watu wangu watajiunga na watu wako katika kazi hiyo, nami nitawalipa watumishi wako kadiri utakavyosema. Maana kama vile unavyojua, hakuna yeyote mwenye kuwa fundi wa kukata miti kama ninyi Wasidoni.” Hiramu alifurahi sana alipopata ujumbe huu wa Solomono, akasema: “Yawe asifiwe wakati huu, kwa kumupa Daudi mwana mwenye hekima atawale taifa hili kubwa.” Kisha, Hiramu alimupelekea Solomono ujumbe, akisema: “Nimepokea ujumbe wako, nami niko tayari kutimiza mahitaji yako juu ya mbao za mierezi na za miberoshi. Watu wangu watasomba magogo na kuyateremusha kutoka Lebanoni mpaka katika bahari na kuyafunga mafungumafungu kusudi yaelee juu ya maji mpaka pahali utakaponielezea. Kule, yatafunguliwa nawe utayapokea. Kwa upande wako, wewe utanipa chakula kwa ajili ya watu wa nyumba yangu.” Basi, Hiramu alimupa Solomono mbao zote za aina ya mierezi na miberoshi alizohitaji, naye Solomono akamupa Hiramu ngano madebe elfu mia mbili na makumi ine, na mafuta safi madebe mia mbili kila mwaka, kwa ajili ya watu wa nyumba yake. Basi, Yawe akamupa Solomono hekima kama alivyomwahidi. Kukakuwa amani kati ya Solomono na Hiramu; wakafanya mapatano kati yao. Mufalme Solomono alikusanya watu elfu makumi tatu kutoka kila pahali katika inchi ya Israeli, wafanye kazi za kulazimishwa, akamuweka Adoniramu akuwe musimamizi wao. Aliwagawanya watu hao katika makundi matatu ya watu elfu kumi kila moja, akayapeleka makundi hayo kwa zamu, mwezi mumoja Lebanoni na miezi miwili kwao. Solomono alikuwa vilevile na wabebaji wa mizigo elfu makumi saba, na wachongaji wa mawe elfu makumi nane kwenye milima, bila kuhesabu wasimamizi elfu tatu na mia tatu waliosimamia kazi hiyo na wafanyakazi wote. Kwa amri ya mufalme, walichimbua mawe makubwa na ya bei kali, kusudi yachongwe kwa ajili ya kujenga musingi wa nyumba. Basi, hivi ndivyo wajengaji wa Solomono na Hiramu na watu wa muji wa Gebali walivyotayarisha mawe na mbao za kujenga nyumba hiyo. Solomono alianza kujenga nyumba ya Yawe katika mwaka wa mia ine na makumi nane kisha Waisraeli kutoka Misri. Huo ulikuwa mwaka wa ine wa utawala wa Solomono juu ya Israeli, katika mwezi wa Zivu, ni kusema mwezi wa pili. Nyumba hiyo ambayo mufalme Solomono alimujengea Yawe ilikuwa na urefu wa metre makumi mbili na saba, upana metre kenda, na metre kumi na tatu na nusu urefu wa kwenda juu. Uwanja wa baraza ya nyumba ulikuwa na upana wa metre ine na nusu toka upande mumoja wa nyumba mpaka upande mwingine. Na kina chake mbele ya hiyo nyumba kilikuwa metre tisa. Aliiwekea nyumba hiyo madirisha mapana kwa ndani na membamba kwa inje. Tena aliongeza kujenga nguzo kuzunguka, kwa kutegemeza ukuta wa inje. Akatengeneza vyumba vya pembeni kila upande. Vyumba vya chini, katika hivyo vyumba vya nyongezo, vilikuwa na upana wa metre mbili na sentimetre makumi mbili na tano, na gorofi iliyofuata ilikuwa na upana wa metre mbili na sentimetre makumi ine na tano, na gorofi ya juu kabisa ilikuwa na upana wa metre tatu. Gorofi hizo zilikuwa zimetofautiana kwa upana, kwa sababu Solomono alikuwa amepunguza kipimo cha ukuta wa inje kuzunguka nyumba, kusudi miti ya kutegemeza jengo isishikamane na kuta. Wakati nyumba ilipokuwa inajengwa, hakukusikilika ndani ya nyumba mulio wa nyundo, wala wa chombo chochote cha chuma, maana ilijengwa kwa mawe yaliyokuwa yamechongwa na kutayarishwa kabisa kule walikoyachimba. Mulango wa kuingilia sehemu ya chini ya jengo lililoongezwa kwenye ubavu wa nyumba, ulikuwa upande wa kusini. Ndani, mulikuwa ngazi ambayo watu waliweza kupandia kwa kwenda kwenye gorofi ya katikati na ya mwisho. Hivyo, Solomono aliijenga nyumba, ikamalizika. Dari ya nyumba alikuwa ameitengeneza kwa boriti na mbao za mierezi. Kuuzunguka ukuta wa inje wa nyumba hiyo, alijenga vyumba kila gorofi ikiwa na urefu wa kwenda juu metre mbili na sentimetre makumi mbili na tano; navyo vilikuwa vimeunganishwa na nyumba kwa boriti za mierezi. Wakati ule, neno la Yawe lilimufikia Solomono kusema hivi: “Juu ya nyumba hii unayoijenga, kama ukifuata masharti yangu, ukiyatii maagizo yangu na amri zangu zote, nitakutimizia mambo yote niliyomwahidi baba yako Daudi. Mimi nitakaa kati ya wazao wa Waisraeli, na sitawaacha hata kidogo watu wangu, Waisraeli.” Hivyo, Solomono akaijenga nyumba na kuimaliza. Upande wa ndani wa kuta za nyumba aliufunika kwa mbao za mierezi, kutokea kwenye sakafu mpaka kwenye boriti za dari; na sakafu akaitandikia mbao za miberoshi. Chumba cha ndani, kilichoitwa Pahali Patakatifu Sana, kilijengwa katika sehemu ya nyuma ya nyumba. Kilikuwa kimejengwa kwa mbao za mierezi kutokea kwenye sakafu mpaka kwenye dari, na urefu wake ulikuwa metre tisa. Nyumba ile iliyokuwa mbele ya Pahali Patakatifu Sana, ilikuwa na urefu wa metre kumi na nane. Mbao za mierezi zilizofunika ukuta wa nyumba kwa ndani zilikuwa zimepambwa kwa michoro ya maboga na maua yaliyochanua. Kila sehemu ilikuwa imefunikwa kwa mbao za mierezi, wala hakuna jiwe lililoonekana. Katika sehemu ya ndani kabisa ya jengo hilo, Solomono alitayarisha chumba cha pekee ambamo Sanduku la Agano la Yawe liliwekwa. Chumba hicho kilikuwa na metre tisa urefu, metre tisa upana, na metre tisa kwenda juu; nacho kilipambwa kwa zahabu safi. Vilevile, alitengeneza mazabahu kwa mbao za mierezi. Solomono aliipamba kwa zahabu safi sehemu ya ndani ya nyumba, na mbele ya hicho chumba cha ndani akaweka minyororo ya zahabu kutoka upande mumoja mpaka upande wa pili, aliipamba kwa zahabu. Nyumba yote aliipamba kwa zahabu, na mazabahu yote iliyokuwa katika chumba cha ndani kabisa. Alitengeneza kwa mbao za mizeituni sanamu za makerubi wawili, kila sanamu ikiwa na metre ine na nusu kwenda juu, akaziweka katika chumba cha ndani kabisa. Kila bawa lilikuwa na urefu wa metre mbili na sentimetre makumi mbili na tano; kwa hiyo urefu kutoka incha ya bawa moja mpaka incha ya bawa lingine ulikuwa metre ine na nusu. Kerubi mwingine alikuwa na urefu wa metre ine na nusu; makerubi wote wawili walikuwa na vipimo vilevile na umbo lilelile. Urefu wa kerubi mumoja ulikuwa metre ine na nusu; vilevile urefu wa kerubi mwingine ulikuwa uleule. Sanamu hizo zilielekeana, zikiwa na mabawa yaliyokunjuliwa: bawa la mumoja likigusa ukuta mumoja, na bawa la mwingine likigusa ukuta wa pili, na yale mengine yaligusana katikati ya chumba. Nazo sanamu hizo alizipamba kwa zahabu. Kuta za kila chumba alizipamba kwa kuchongwa michoro ya makerubi, miti ya ngazi na michoro ya maua yaliyochanua. Aliipakaa zahabu kwenye sakafu ya vyumba vya ndani na vya inje. Kwa kuingilia katika chumba cha ndani kabisa alitengeneza milango kwa mbao za mizeituni. Vizingiti na miimo ya milango vilifanya umbo la pembe tano. Katika milango hiyo miwili ya mizeituni, alichora makerubi, miti ya ngazi na maua yaliyochanua; akaipamba michoro hiyo kwa zahabu. Vilevile, alitengeneza mulango wa muraba wa kuingilia katika baraza. Miimo ya mulango huo ilikuwa ya mizeituni, na mbao zake mbili zilikuwa za miberoshi; kila ubao uliweza kukunjwa mara moja. Juu ya mbao hizo za mulango, kulichorwa makerubi, miti ya ngazi na maua yaliyochanua; akaipamba vizuri michoro hiyo kwa zahabu. Alijenga uwanja wa ndani ambao kuta zake zilikuwa za mistari tatu ya mawe yaliyochongwa, na mustari moja wa boriti za mwerezi. Musingi wa nyumba ya Yawe ulijengwa katika mwezi wa Zivu, katika mwaka wa ine. Na katika mwezi wa Buli, ni kusema mwezi wa nane, katika mwaka wa kumi na mumoja, ujenzi wa nyumba ulimalizika, na kazi ilikuwa imekamilika kama ilivyopangwa. Solomono alitumia miaka saba kwa kujenga. Solomono alijijengea nyumba ya kifalme, naye alitumia muda wa miaka kumi na mitatu kwa kuimaliza. Kisha, akajenga jengo lililoitwa Nyumba ya pori ya Lebanoni. Urefu wake ulikuwa metre makumi ine na ine na nusu, upana wake metre makumi mbili na mbili na sentimetre makumi mbili na tano, na urefu wake wa kwenda juu metre kumi na tatu na nusu. Ilikuwa imejengwa juu ya mistari mitatu ya nguzo za mierezi, nguzo ambazo zilishikilia boriti za mierezi kwa upande wa juu. Kila mustari ulikuwa na nguzo kumi na tano; basi zote pamoja zilikuwa nguzo makumi ine na tano. Vyumba vilivyojengwa juu ya nguzo hizo, alivitilia dari ya mbao za mierezi. Kulikuwa mistari mitatu ya madirisha yaliyoelekeana. Milango yote ilikuwa ya muraba, na miimo ya madirisha hayo yaliyoelekeana ilikuwa ya muraba vilevile. Alijenga uwanja wa nguzo, ambao urefu wake ulikuwa metre makumi mbili na mbili na sentimetre makumi mbili na tano, na upana wake metre kumi na tatu na nusu. Kwenye sehemu ya mbele ya jengo hilo kulikuwa baraza. Mbele ya baraza kulikuwa nguzo; na mbele ya nguzo kulitokeza paa dogo. Solomono alijenga uwanja wa kiti cha kifalme ambamo aliamulia maneno ya watu. Huu uliitwa vilevile Uwanja wa Hukumu. Ulipambwa kwa mbao za mierezi kutoka sakafu mpaka dari. Nyumba yake ya kukaa mwenyewe iliyokuwa nyuma ya Uwanja wa Hukumu. Ilijengwa kama zile zingine. Solomono alijenga vilevile nyumba kama uwanja huo kwa ajili ya binti ya mufalme wa Misri, ambaye alikuwa amemwoa. Majengo hayo yote yalijengwa kwa mawe ya bei kali kutoka musingi mpaka juu, mawe ambayo yalikuwa yamechongwa kwa vipimo vilivyoamuriwa, na kukatwa kwa musumeno upande wa ndani na wa inje. Musingi ulikuwa wa mawe ya bei kali na makubwa yenye urefu wa metre tatu na nusu, na upana metre ine na nusu. Sehemu za juu zilijengwa kwa mawe mengine yaliyochongwa kwa vipimo vilivyoamuriwa, na kwa mbao za mierezi. Kiwanja cha nyumba ya mufalme kilikuwa na kuta zenye mustari moja wa mbao za mierezi na mistari mitatu ya mawe ya kuchongwa kila moja; ndivyo ilivyokuwa hata kwa kiwanja cha ndani cha nyumba ya Yawe na kwa baraza la nyumba. Kisha mufalme Solomono alimwita Hiramu kutoka Tiro. Huyo alikuwa mwana wa mujane wa kabila la Nafutali, na baba yake alikuwa mukaaji wa Tiro, mufua-shaba. Hiramu alikuwa na hekima nyingi na akili, fundi kabisa wa kazi yoyote ya shaba. Basi, alikuja kwa mufalme Solomono, akamufanyia kazi yake yote. Hiramu alitengeneza nguzo mbili za shaba, kila moja ikiwa na urefu wa metre ine, na muzunguko wa metre tano na nusu. Ndani zilikuwa na tundu ambalo unene wa pande zake ulikuwa sentimetre mbili. Halafu akatengeneza taji mbili za shaba, kila moja ikiwa na urefu wa kwenda juu wa metre mbili na sentimetre makumi mbili na tano. Akaziweka juu ya nguzo hizo. Halafu, alifuma nyavu mbili zenye mapambo ya murabamuraba, akatengeneza taji kwa kusokota mukufu: vyote hivyo kwa ajili ya kupamba taji za shaba zilizowekwa juu ya zile nguzo. Vilevile, alitengeneza matunda aina ya makomamanga, akayapanga kwa mistari miwili kuzunguka zile taji juu ya kila nguzo. Na taji hizo zilizokuwa juu ya nguzo mbele ya baraza, zilipambwa kwa mufano wa maua ya yungiyungi, urefu wa kwenda juu metre moja na sentimetre makumi munane. Taji hizo zilikuwa juu ya hizo nguzo mbili, na vilevile zilikuwa juu ya sehemu ya muviringo iliyojitokeza karibu na zile nyavu. Kulikuwa mifano mia ine ya matunda ya makomamanga, imepangwa kwa mistari miwili kuzunguka kila taji. Hiramu aliziweka nguzo hizo kwenye baraza ya hekalu; nguzo aliyoisimika upande wa kusini iliitwa Yakini, na ile aliyoisimika upande wa kaskazini iliitwa Boazi. Vichwa vya nguzo hizo vilipambwa kwa mufano wa maua ya yungiyungi. Na hivyo kazi ya kutengeneza nguzo ikamalizika. Hiramu alitengeneza birika la maji la muviringo lenye upana wa metre ine na nusu kutoka ukingo mpaka ukingo, na urefu wa metre mbili na sentimetre makumi mbili na muzunguko wa metre kumi na tatu na nusu. Chini ya ukingo wake, kulizunguka birika hilo, kulikuwa mistari miwili ya vibuyu, kila kimoja metre kumi na tatu na nusu. Vibuyu hivyo vilikuwa vimetengenezwa wakati uleule birika lile lilipofanywa. Nalo birika lilikuwa limewekwa juu ya sanamu za ngombe dume kumi na wawili; tatu zikielekea upande wa kaskazini, tatu zikielekea upande wa magaribi, tatu kusini, na nyingine tatu mashariki. Birika liliwekwa juu ya ngombe dume hao, sehemu zao za nyuma zikiwa ndani. Unene wa ukingo wake ulikuwa sentimetre saba na nusu; nao ulikuwa ukifanana na ukingo wa kikombe na kama ua la yungiyungi. Birika liliweza kujaa maji kadiri ya litre elfu makumi ine. Hiramu alitengeneza vilevile magari kumi ya shaba, kila gari likiwa na urefu wa metre moja na sentimetre makumi nane, upana wa metre moja na sentimetre makumi nane, na urefu wa kwenda juu metre moja na sentimetre makumi mbili. Magari hayo yalikuwa yameundwa hivi: kulikuwa vibandiko vya chuma ambavyo vilikuwa vimeshikiliwa na mitalimbo. Juu ya vibandiko vile vilivyoshikiliwa na mitalimbo, kulikuwa sanamu za simba, ngombe dume na makerubi. Sanamu hizo za simba na ngombe dume, zilikuwa zimefunikwa na kutandikwa juu ya mapambo yaliyosokotwa vizuri. Kila gari lilikuwa na magurudumu mane ya shaba, na vyuma vya katikati vya kuyashika magurudumu hayo, vilikuwa vya shaba. Kwenye pembe ine za gari kulikuwa vikingio vya shaba kwa ajili ya birika kubwa. Karibu ya kila kikingio kuliwekwa mapambo ya maua ya kusokotwa. Mulango wa gari ulikuwa katika sehemu iliyotokeza juu kwa kipimo cha nusu metre. Kwa inje, mulango ulikuwa umetiwa michoro; na vibandiko vyake vilikuwa vya muraba, si ya muviringo. Na hayo magurudumu mane yalikuwa chini ya vile vibandiko; vyuma vya katikati kwa kushika magurudumu hayo vilikuwa vimeunganishwa na majengo ya gari lenyewe; na urefu wa kwenda juu wa magurudumu hayo ulikuwa sentimetre makumi saba na tano. Hayo magurudumu yalikuwa kama magurudumu ya magari ya vita; na vyuma vyake vya katikati, kingo zake za miviringo, sambo zake na vyuma vya ndani: hivyo vyote vilikuwa vya shaba iliyoyeyushwa. Chini ya kila gari kulikuwa vikingio vine kwenye pembe zake, navyo vilifungamana na gari. Na juu ya kila gari kulikuwa muviringo wa sentimetre makumi mbili na tano kwenda juu; na vikingio na vibandiko vilivyokuwa upande wa juu vilishikamana na gari lenyewe. Kwenye nafasi wazi iliyopatikana katika vikingio na vibandiko vya kila gari, Hiramu alichonga michoro ya makerubi, simba na miti ya ngazi, akazungusha mashada ya mapambo. Mifano hiyo yote kumi ya magari ilifanana, ikiwa na kimo kimoja na umbo lilelile. Hiramu alitengeneza vilevile mabeseni kumi ya shaba, moja kwa kila gari. Kila beseni ilikuwa na upana wa metre moja na sentimetre makumi ine na tano, na iliweza kujaa maji kadiri ya litre elfu moja na mia sita. Akaweka magari matano upande wa kusini wa nyumba, na matano upande wa kaskazini; na birika akaliweka kwenye pembe ya kusini-mashariki ya nyumba. Vitu hivyo vyote mufalme alivitengeneza katika kiwanda cha Yordani, sehemu ya udongo wa mufinyanzi iliyokuwa kati ya Sukoti na Zaretani. Solomono hakupima uzito wa vifaa hivi vyote kwa kuwa vilikuwa vingi sana, na kwa sababu uzito wa shaba haukujulikana. Basi, mufalme Solomono akamaliza kazi zote zilizoelekea nyumba ya Yawe. Kisha Solomono akaleta mali yote ambayo baba yake Daudi, alikuwa ameitoa kwa Bwana, ni kusema: feza, zahabu na vyombo; akaiweka katika hazina za nyumba ya Yawe. Basi, mufalme Solomono akawakusanya mbele yake kule Yerusalema wazee na viongozi wote wa makabila na wa ukoo za Waisraeli kusudi waliondoe Sanduku la Agano la Yawe katika muji wa Daudi, ni kusema Sayuni. Halafu watu hao wote wakakusanyika mbele ya mufalme Solomono wakati wa sikukuu ya mwezi wa Etanimu, ni kusema mwezi wa saba. Kisha kufika kwa wazee wote wa Israeli, makuhani walibeba Sanduku la Agano. Walawi na makuhani walihamisha Sanduku la Agano na hema la mukutano, na vyombo vitakatifu vyote vilivyokuwa mule ndani ya hema. Mufalme Solomono na mukutano wote wa Israeli wakakusanyika mbele ya Sanduku la Agano, nao wakatoa sadaka: ngombe na kondoo wasiohesabika. Kisha makuhani wakaliingiza Sanduku la Agano la Yawe kwa nafasi yake katika chumba cha ndani cha nyumba, ni kusema Pahali Patakatifu Sana, chini ya mabawa ya makerubi. Hao makerubi walitandaza mabawa yao juu ya pahali Sanduku lilipowekwa, juu ya Sanduku ile na miti yake ya kulibebea. Kwa sababu miti hiyo ilikuwa mirefu sana, incha zake ziliweza kuonekana kutoka Pahali Patakatifu, mbele ya chumba cha ndani; lakini haikuweza kuonekana kutoka upande wa inje. Miti hiyo ingali pahali pale hata leo. Hakukukuwa kitu ndani ya Sanduku la Agano lakini vile vibao viwili vya mawe ambavyo Musa aliviweka mule kule Horebu, pahali Yawe alipofanya agano na Waisraeli walipotoka katika inchi ya Misri. Makuhani walipotoka pale Pahali Patakatifu, wingu liliijaza nyumba ya Yawe. Nao makuhani walishindwa kutumika ndani kwa sababu ya wingu hilo; kwa sababu utukufu wa Yawe uliijaza nyumba ya Yawe. Halafu Solomono akasema: “Yawe alisema kwamba atakaa katika giza nene. Hakika, nimekujengea nyumba ya kukaa, pahali pa makao yako ya milele.” Kisha, Solomono akawaelekea Waisraeli wote walipokuwa wakisimama, akawabariki, akasema: “Atukuzwe Yawe, Mungu wa Israeli, maana kwa nguvu yake ametimiza ahadi yake aliyomupa baba yangu Daudi, akisema: ‘Tangu nilipowaondoa watu wangu Waisraeli katika inchi ya Misri, sikuchagua muji wowote katika makabila ya Waisraeli kusudi nijengewe nyumba nitakamoabudiwa; lakini nilimuchagua Daudi, atawale watu wangu, Waisraeli.’ Kwa hiyo, baba yangu alikusudia kumujengea Yawe, Mungu wa Israeli nyumba. Lakini Yawe alimwambia baba yangu Daudi: ‘Ni vizuri kwamba ulikusudia ndani ya moyo wako kunijengea nyumba. Hata hivyo, si wewe utakayenijengea nyumba, lakini ni mwana wako utakayemuzaa ndiye atakayenijengea hiyo nyumba.’ Na sasa, Yawe ametimiza ahadi yake, maana nimekuwa mufalme pahali pa baba yangu Daudi, na kukiikalia kiti cha kifalme cha Israeli kama vile Yawe alivyoahidi. Tena nimejenga nyumba ya kumwabudia Yawe, Mungu wa Israeli. Zaidi ya hayo, nimetenga nafasi ya kuweka Sanduku la Agano ambalo ndani yake muko agano Yawe alilofanya na babu zetu, wakati alipowatoa katika inchi ya Misri.” Kisha Solomono alisimama kwenye mazabahu ya Yawe, mbele ya Waisraeli wote, aliinua mikono yake juu, akasema: “Ee Yawe, Mungu wa Israeli, hakuna Mungu mwingine kama wewe, juu mbinguni, au chini katika dunia. Wewe unashika agano lako na kutenda wema kwa watumishi wako wanaoishi wakikutii kwa moyo wao wote. Umetimiza ahadi uliyoitoa kwa mutumishi wako Daudi baba yangu; hakika, yale uliyosema umeyatimiza leo kwa uwezo wako mwenyewe. Kwa hiyo, sasa, ee Yawe, Mungu wa Israeli, ninakuomba vilevile utimize ile ahadi uliyomwahidi mutumishi wako Daudi, baba yangu, ukisema: ‘Siku zote utakuwa na mutu mumoja wa uzao wako kwa kuikaa katika kiti cha kifalme cha Israeli, ikiwa wazao wako watakuwa waangalifu juu ya mwenendo wao mbele yangu kama wewe ulivyofanya mbele yangu.’ Basi, ee Mungu wa Israeli, ninakusihi utimize hayo yote uliyomwahidi mutumishi wako Daudi, baba yangu. “Lakini, ee Mungu, kweli utakaa katika dunia? Ikiwa hata mbingu zenyewe wala mbingu za juu sana hazikutosha, namna gani nyumba hii ambayo nimeijenga itakutoshelea? Hata hivyo, ee Yawe, Mungu wangu, unigeukie mimi mutumishi wako ninapokuomba na kukusihi. Usikilize malalamiko na maombi ambayo mimi mutumishi wako ninaomba leo. Uchunge nyumba hii usiku na muchana, nafasi ambapo umesema: ‘Hapo ndipo watu watakapoliheshimu jina langu’. Unisikilize ninapokuja pahali hapa kwa kuomba. Usikilize wakati tunapokusihi, mimi mutumishi wako na watu wako Waisraeli ambao tutaomba tukielekea pahali hapa. Kutokea kwako mbinguni, usikilize. Na ukisha kusikiliza, utusamehe. “Mutu akimukosea mwenzake, naye akiletwa apate kuapa mbele ya mazabahu yako katika nyumba hii, naye akiapa, tafazali wewe usikilize kutokea kule mbinguni, utende na kuwahukumu watumishi wako. Anayekuwa na kosa umwazibu kwa kadiri ya makosa yake; asiyekuwa na kosa umwachilie na kumupatia haki kwa kadiri ya haki yake. “Ikiwa watu wako Waisraeli wameshindwa na waadui zao kwa sababu ya zambi walizotenda mbele yako, nao wakikugeukia na kusifu jina lako, wakiomba na kukusihi katika nyumba hii, basi, uwasikilize kutokea kule mbinguni, uwasamehe watu wako Waisraeli zambi zao, halafu uwarudishe katika inchi uliyowapa babu zao. “Mvua isiponyesha kwa sababu wametenda zambi mbele yako na unawaazibu, wakiomba wakielekea pahali hapa na kusifu jina lako, vilevile wakiziacha zambi zao na kukurudilia, tafazali, uwasikilize kutokea kule mbinguni, usamehe zambi za watumishi wako, watu wako Waisraeli, na uwafundishe kufuata njia nzuri. Kisha unyeshe mvua katika inchi yako hii ambayo uliwapa watu wako kwamba itakuwa mali yao. “Ikiwa kuna njaa katika inchi, au ugonjwa mukali, ukosefu wa mvua, ugonjwa wa mimea, nzige au vidudu vingine, au ikiwa watu wako wameshambuliwa na waadui zao katika muji wao wowote, ikiwa kuna pigo lolote au ugonjwa wowote, tafazali, chochote ambacho mutu yeyote au watu wako wote wa Waisraeli wanakuomba na kukusihi, kila mutu akijua taabu ndani ya moyo wake na kunyoosha mikono yake kuelekea nyumba hii, basi, usikilize kule kwako mbinguni, uwasamehe na kumutendea kila mutu kwa kadiri anavyostahili, maana ni wewe tu unayejua mawazo ya mioyo ya wanadamu wote, kusudi wakutii wakati wote wanapoishi katika inchi uliyowapa babu zetu. “Hata wakati mugeni asiyekuwa mumoja wa watu wako Waisraeli akikuja kutoka inchi ya mbali kwa ajili ya jina lako, maana watu wa mataifa mengine watasikia sifa zako na juu ya nguvu na uwezo wako, mutu yule akikuja na kuomba akielekea nyumba hii, usikilize kutokea kwako mbinguni. Umujalie yule mugeni yote atakayokulilia, kusudi watu wote katika ulimwengu wapate kujua jina lako na kukutii kama watu wako Waisraeli wanavyofanya, na wapate kufahamu kwamba nyumba hii ambayo nimeijenga, inajulikana kwa jina lako. “Watu wako wakienda kwa vita kupigana na adui yao kwa upande wowote utakapowapeleka, nao wakikuomba wakielekea muji uliouchagua na nyumba niliyoijenga kwa ajili ya jina lako, usikilize kutoka mbinguni wanapokuomba na kukusihi. Uwapatie ushindi katika vita. “Ikiwa watatenda zambi mbele yako, maana hakuna mutu asiyetenda zambi, nawe ukiwakasirikia na kuwaacha washindwe na adui, hata wapelekwe mateka mpaka katika inchi ya adui inayokuwa mbali au karibu, kama watakapokuwa kule katika uhamisho wakijifikiri ndani yao wenyewe na kukugeukia, kama katika ile inchi ya uhamisho wakikusihi na kusema ‘Tumetenda zambi; tumepotoka na kufanya maovu’, vilevile wakati ule watakapokuwa katika inchi ya waadui zao, wakikugeukia kwa moyo wao wote na kwa roho yao yote, na kama wakikuomba wakielekea inchi yao ambayo uliwapatia babu zao, wakielekea muji huu ambao uliuchagua na nyumba hii ambayo nimeijenga kwa ajili ya jina lako, basi, kutoka kwako mbinguni usikilize wakati wanakuomba na kukusihi. Uwasaidie. Uwasamehe watu wako zambi walizotenda mbele yako na uasi wao, uwahurumie mbele ya waadui zao, kusudi nao wapate kuwahurumia, maana ni watu wako, na ni mali yako, watu ambao uliwatoa Misri kutoka katika furu ya chuma. “Uangalie wakati mutumishi wako anapokusihi na wakati watu wako Waisraeli wanapokusihi. Uwasikilize kila mara wanapokulilia. Kwa sababu, ee Bwana wetu Yawe, uliwatenga na watu wa mataifa mengine katika dunia, kusudi wakuwe mali yako, kama ulivyotangaza kwa njia ya Musa, mutumishi wako, wakati ule ulipowatoa babu zetu katika inchi ya Misri.” Solomono alipomaliza kusema maombi hayo yote na ombi lake kwa Yawe, alisimama kutoka pale mbele ya mazabahu ya Yawe, pahali alipokuwa amepiga magoti akiinua mikono yake juu. Alisimama, akawabariki Waisraeli wote waliokuwa wamekusanyika pale, akisema kwa sauti kubwa: “Atukuzwe Yawe ambaye amewapatia watu wake Waisraeli amani, kulingana na ahadi yake. Ametimiza ahadi zake zote njema alizozitoa kupitia kwa mutumishi wake Musa. Yawe, Mungu wetu, akuwe nasi kama alivyokuwa na babu zetu. Tunaomba asituachilie, wala asitutupilie. Yeye aelekeze mioyo yetu kwake, kusudi tufuate njia zake, tukishika amri zake, masharti yake na maagizo yake aliyowapa babu zetu. Basi, maneno yangu haya ambayo ni ombi langu mbele ya Yawe, yakuwe karibu na Yawe, Mungu wetu, muchana na usiku, naye amujalie mutumishi wake, na watu wake Waisraeli, kusudi wafanikiwe katika mahitaji yao ya kila siku. Nayo mataifa yote katika ulimwengu yatajua kwamba kweli Yawe ndiye Mungu wala hakuna mwingine. Nanyi, mukuwe waaminifu kwa Yawe, Mungu wetu, mukifuata masharti yake na kutii amri zake zote kama munavyofanya hivi leo.” Kisha, mufalme Solomono na Waisraeli wote waliokuwa pamoja naye walimutolea Yawe sadaka. Naye Solomono alimutolea Yawe sadaka za amani: ngombe elfu makumi mbili na mbili na kondoo elfu mia moja na makumi mbili. Hivi ndivyo mufalme na watu wote wa Israeli walivyozindua nyumba ya Yawe. Siku hiyohiyo, mufalme aliizindua sehemu ya katikati ya uwanja uliokuwa mbele ya nyumba ya Yawe, maana ni pale ndipo alipotolea sadaka za kuteketezwa, sadaka za ngano, na mafuta ya sadaka za amani, kwa sababu ile mazabahu ya shaba haikutosha kwa sadaka hizo zote. Naye Solomono kwa muda wa siku saba alifanya sikukuu pamoja na Waisraeli wote. Nao walitoka tangu kwenye kiingilio cha Hamati, mpaka muto wa Misri. Katika siku ya nane, Solomono aliwaaga watu; nao wakamutakia mufalme baraka, wakaenda kwao wakishangilia na kufurahi kwa sababu ya wema ambao Yawe aliuonyesha kwa Daudi, mutumishi wake, na kwa watu wake Waisraeli. Mufalme Solomono alipomaliza kujenga nyumba ya Yawe na nyumba ya kifalme na majengo mengine yote aliyokusudia kujenga, Yawe alimutokea tena kama alivyomutokea kule Gibeoni. Yawe alimwambia: “Nimesikiliza wakati uliponiomba na kunisihi. Nimeitakasa nyumba hii ambayo umenijengea kusudi watu waabudu jina langu hapa milele. Nitaichunga na kuipenda wakati wote. Nawe kama ukinitumikia kwa ukamilifu wa moyo na usawa kama baba yako Daudi alivyofanya, ukitii amri zangu na kutimiza yale yote niliyokuamuru, ukifuata masharti yangu na maagizo yangu, basi, mimi nitakiimarisha kiti chako cha kifalme juu ya Israeli milele, kama nilivyomwahidi baba yako Daudi, nikisema: Hautakosa mutu wa kuikaa juu ya kiti cha kifalme cha Israeli. Lakini wewe au watoto wako mukigeuka na kuacha kunifuata, musiposhika amri zangu na masharti niliyowapa, mukienda kutumikia miungu mingine na kuiabudu, basi, nitawahamisha watu wangu, Waisraeli, kutoka inchi hii ambayo nimewapa; vilevile na nyumba hii ambayo niliyoitakasa kwa ajili ya jina langu, nitaitupilia mbali nami, na kuifanya kitu cha kuchekelewa na kuzarauliwa kati ya watu wa mataifa yote. Na nyumba hii itaharibiwa na kuwa mabomoko. Kila mutu atakayepita karibu atashituka na kutikisa kichwa, na kuuliza: ‘Kwa nini Yawe amefanya hivyo kwa inchi hii na kwa nyumba hii?’ Watu wengine watajibu: ‘Ni kwa sababu walimwacha Yawe, Mungu wao, aliyewatoa babu zao katika inchi ya Misri, wakashikamana na miungu mingine, wakaiabudu na kuitumikia; kwa hiyo, Yawe amewaletea hasara hizi zote.’ ” Kisha miaka makumi mbili ambayo Solomono alipitisha kwa kuzijenga nyumba ya Yawe na nyumba ya kifalme, mufalme Solomono alimupa Hiramu mufalme wa Tiro miji makumi mbili katika jimbo la Galilaya kwa sababu yule Hiramu alikuwa amemupelekea Solomono mbao za mierezi na miberoshi, na zahabu vilevile, kadiri alivyohitaji kwa majengo. Lakini Hiramu alipofika kutoka Tiro na kuiona miji hiyo aliyokuwa amepewa na Solomono hakupendezwa nayo. Basi, akamwuliza Solomono: “Ndugu yangu, ni miji gani hii ambayo umenipa?” Ndiyo sababu miji hiyo inaitwa “Inchi ya Kabure” hata leo. Hiramu alikuwa amemupelekea mufalme Solomono zahabu kilo elfu tatu na mia sita. Haya ni maelezo juu ya mufalme Solomono, jinsi alivyowatumikisha watu kazi za kulazimishwa katika kujenga nyumba ya Yawe, nyumba yake ya kifalme, uwanja wa Milo, na ukuta wa Yerusalema, na vilevile katika kujenga upya miji ya Hazori, Megido na Gezeri. Gezeri ndio muji ambao mufalme wa Misri alikuwa ameuteka, akauchoma kwa moto na kuwaua Wakanana, wakaaji wake. Nyuma, binti wa mufalme wa Misri alipoolewa na Solomono, mufalme wa Misri alimupa binti yake muji ule wa Gezeri ukuwe zawadi ya arusi. Basi, Solomono aliujenga upya muji wa Gezeri. Vilevile alijenga Beti-Horoni wa chini; tena miji hii: Balati, na Tamari, muji unaokuwa katika mbuga katika inchi ya Yuda, na miji yake yote ya kuwekea akiba, magari yake ya vita, na waaskari wapanda-farasi wake; vilevile na chochote alichotaka kujenga katika Yerusalema, Lebanoni au nafasi ingine katika ufalme wake. Watu wengine wote waliobaki kati ya Waamori, Wahiti, Waperizi, Wahivi na Wayebusi, maana yake wote hao ambao hawakukuwa wa taifa la Israeli, pamoja na wazao wao ambao Waisraeli hawakuweza kuwaangamiza kabisa, Solomono aliwatumikisha kazi za kulazimishwa hata leo. Lakini kati ya Waisraeli, Solomono hakumufanya mutu hata mumoja kuwa mutumwa. Waisraeli walimutumikia kwa kuwa waaskari, waongozi, majemadari, wakubwa, wasimamizi wa magari yake ya vita, na waaskari wapanda-farasi. Hii ndiyo jumla ya wakubwa waliohusika na uangalizi wa kazi ya Solomono: watu mia tano na makumi tano, hao ndio waliosimamia watu waliofanya kazi. Kisha binti ya mufalme wa Misri alihama katika muji wa Daudi, akaenda kukaa katika nyumba yake mwenyewe ambayo Solomono alimujengea. Kisha Solomono akajenga uwanja wa Milo. Mara tatu kila mwaka, Solomono alitoa sadaka za kuteketezwa na sadaka za amani juu ya mazabahu aliyokuwa amemujengea Yawe, akamufukizia Yawe ubani. Akafanya vile ilivyofaa kwa nyumba ya Yawe. Mufalme Solomono alitengeneza mashua nyingi kule Ezioni-Geberi, karibu na Eloti kwa kivuko cha bahari Nyekundu, katika inchi ya Edomu. Naye mufalme Hiramu akawatuma wafundi wake wenye kujua bahari pamoja na watumishi wa Solomono. Walisafiri kwenda katika inchi ya Ofiri, na kuleta toka kule zahabu, wakamuletea mufalme Solomono yapata kilo elfu kumi na ine. Malkia wa Seba aliposikia sifa za Solomono, kwa sababu ya jina la Yawe, alimwendea Solomono kwa kumujaribu kwa maulizo magumu. Akafika Yerusalema akisindikizwa na watu wengi sana pamoja na ngamia waliobeba marasi, zawadi nyingi sana, zahabu na mawe ya bei kali. Naye Solomono akayajibu maulizo yote; hakuna hata ulizo moja lililomushinda. Malkia wa Seba alishangaa sana alipoiona hekima yote ya Solomono, na nyumba aliyokuwa ameijenga, tena alipoona chakula kilicholetwa kwa meza yake, jinsi wakubwa wake walivyoikaa kwenye meza, jinsi watumishi walivyotumika na walivyovaa, vilevile wenye kuleta vinywaji na sadaka za kuteketezwa ambazo alizitoa katika nyumba ya Yawe, alipumbazika na kushangaa sana. Basi, akamwambia mufalme: “Mambo yote niliyosikia katika inchi yangu juu ya kazi zako na hekima yako ni kweli! Lakini sikuweza kuamini habari hizo mpaka nilipofika na kujionea mwenyewe. Kumbe sikuambiwa hata nusu yake; hekima yako na fanaka zako vimepita habari nilizopewa. Heri kwa wake zako! Heri kwa hawa watumishi wako ambao wanakutumikia siku zote na kusikiliza hekima yako! Asifiwe Yawe, Mungu wako, ambaye amependezwa nawe, akakuweka juu ya kiti cha kifalme cha Israeli! Kwa sababu Yawe anapenda Israeli milele, amekuweka wewe ukuwe mufalme, kusudi uimarishe haki na sheria ya Mungu.” Kisha malkia akamupa mufalme zaidi ya kilo elfu ine za zahabu, marasi nyingi sana na mawe ya bei kali. Hakuna aliyeweza hata kidogo kumuletea mufalme Solomono marasi mengi sana sawa yale malkia wa Seba aliyomuletea. Tena, mashua za Hiramu zilizoleta zahabu kutoka Ofiri, zilileta kwa wingi miti ya musandali na mawe ya bei kali. Naye mufalme aliitumia miti hiyo ya musandali kwa ajili ya nguzo za nyumba ya Yawe, na za nyumba ya kifalme na vilevile kwa kutengeneza vinubi na vinanda vya waimbaji. Kiasi cha miti ya musandali kama hicho hakijaonekana tena mpaka leo. Mufalme Solomono naye alimupatia malkia wa Seba kila kitu alichotamani na alichotaka, pamoja na vitu vingine ambavyo Solomono alimupa kutokana na desturi yake ya kifalme. Basi malkia akarudi kwake pamoja na watumishi wake. Kila mwaka, Solomono alipelekewa zahabu kilo elfu makumi mbili na mbili. Kiasi hicho si pamoja na zahabu aliyopata kwa wafanyabiashara na wachuuzi, kwa wafalme wote wa Arabia na watawala wa inchi ya Israeli. Mufalme Solomono alitengeneza ngao kubwa mia mbili kwa zahabu iliyofuliwa; kila ngao kilo saba za zahabu. Alitengeneza ngao ndogondogo mia tatu kwa zahabu iliyofuliwa; kilo moja na nusu ilitumiwa kwa kila ngao. Halafu mufalme akaziweka katika jengo lililoitwa Nyumba ya Pori ya Lebanoni. Vilevile mufalme alitengeneza kiti cha kifalme kikubwa cha pembe, akakipakaa zahabu safi kabisa. Kiti hicho kilikuwa na ngazi sita. Sehemu ya juu ilikuwa imeviringwa na kiliwekewa pahali pa kuegemeza mukono pande zake mbili; na sanamu za simba wawili wamesimama mumoja pembeni ya pahali pale pa kuegemeza mukono. Kulikuwa vilevile sanamu kumi na mbili za simba wamesimama, mumoja kwa mwisho wa kila ngazi. Kiti kama hicho kilikuwa bado hakijatengenezwa katika ufalme wowote. Vyombo vyote vya kunywa divai vya mufalme Solomono vilikuwa vya zahabu, na vyombo vyote vilivyokuwa katika Nyumba ya Pori ya Lebanoni vilikuwa vya zahabu safi; hakuna kilichotengenezwa kwa feza maana madini ya feza haikuhesabiwa kuwa kitu wakati ule. Kwa sababu mufalme Solomono alikuwa na mashua kubwa za Tarsisi zilizokuwa zikisafiri pamoja na mashua za Hiramu, kisha kila miaka mitatu mashua hizo za Tarsisi zilimuletea mufalme zahabu, feza, pembe, kima, na tausi. Mufalme Solomono aliwapita wafalme wote katika dunia kwa mali na hekima. Watu wa inchi zote walikuwa na hamu ya kumwendea Solomono kwa kusikiliza hekima yake ambayo Mungu alikuwa amemujalia. Kila mumoja wao alimuletea zawadi: vyombo vya feza, vya zahabu, nguo, manemane, manukato, farasi na nyumbu. Zawadi hizi alizipokea kila mwaka. Solomono alikusanya magari ya vita na waaskari wapanda-farasi. Alikuwa na magari ya vita elfu moja na mia ine na waaskari wapanda-farasi elfu kumi na mbili ambao aliwaweka katika miji yenye vituo vya magari ya vita, na kule Yerusalema. Basi, Solomono alifanya feza katika Yerusalema kuwa kitu cha kawaida kama mawe, na mbao za mierezi zilikuwa nyingi kama mbao za mikuyu ya Shefela. Solomono aliagiza farasi kutoka Misri, na vilevile kutoka Kilikia ambako wachuuzi wake waliwanunua. Gari moja liliweza kununuliwa kule Misri kwa feza inayopita kilo saba, na farasi mumoja aliweza kununuliwa kwa feza kilo mbili. Wachuuzi wa mufalme walisafirisha magari na farasi hao na kuwauzishia wafalme wote wa Wahiti na wa Waaramu. Solomono alipenda sana wanawake wa kigeni: binti ya mufalme wa Misri, wanawake wa Wamoabu, Waamoni, Waedomu, Wasidoni, na Wahiti, ni kusema wanawake wa mataifa ambayo Yawe alikuwa amewakataza Waisraeli akisema: “Musioe kwao wala wao wasioe kwenu kwa sababu wanawake hao watapotosha mioyo yenu kusudi muitumikie miungu yao.” Solomono aliwapenda sana wanawake hao. Solomono akakuwa na wanawake mia saba, wote wabinti wa kifalme, na wahabara mia tatu. Hao wanawake wakamupotosha. Maana, alipokuwa muzee, wake zake walimupotosha hata akaitumikia miungu mingine, wala hakukuwa mwaminifu kabisa kwa Yawe, Mungu wake, kama baba yake Daudi alivyokuwa mwaminifu. Solomono alimutumikia Astaroti aliyekuwa mungu wa Wasidoni, na alimufuata Milkomu, mungu wa chukizo wa Waamoni. Hivyo, Solomono alitenda maovu mbele ya Yawe, wala hakufuata kwa ukamilifu mapenzi ya Yawe kama baba yake Daudi alivyokuwa amefanya. Juu ya mulima unaokuwa upande wa mashariki wa Yerusalema, Solomono alijenga pahali pa kumutambikia Kemosi, mungu wa chukizo wa Wamoabu, na nafasi ya kumutambikia Milkomu, mungu wa chukizo wa Waamoni. Vilevile, aliwajengea wake zake wote wa kigeni nafasi ya kufukizia ubani na kuitambikia miungu yao. Basi, Yawe alimukasirikia Solomono, kwa sababu alikuwa amemwacha Yawe, Mungu wa Israeli, ingawa yeye alikuwa amemutokea mara mbili na kumwamuru asiiabudu miungu ya kigeni. Solomono hakutii amri ya Yawe. Kwa hiyo Yawe akamwambia Solomono: “Kwa kuwa umeamua kufanya hivyo, ukavunja agano langu nawe, na kuasi masharti yangu niliyokupa, hakika nitakunyanganya huo utawala na kumupa mutumishi wako. Hata hivyo, kwa ajili ya baba yako Daudi, sitafanya hivyo wakati ungali unaishi, lakini nitauondoa utawala huo katika mikono ya mwana wako. Hata yeye sitamunyanganya urizi wote, lakini nitamwachia mwana wako kabila moja, kwa ajili ya mutumishi wangu Daudi, na kwa ajili ya Yerusalema ambao nimeuchagua kuwa wangu.” Halafu Yawe akamufanya Hadadi, aliyekuwa wa ukoo wa mufalme wa Edomu, kuwa adui ya Solomono. Wakati Daudi alipowaangamiza Waedomu, Yoabu, jemadari wa waaskari wa Daudi, alikwenda kule kuwazika waliouawa. Yoabu aliwaua wanaume wote wa Edomu. Yoabu alikaa kule na waaskari wake kwa muda wa miezi sita, apate kuwaangamiza kabisa wanaume wote wa Edomu. Lakini Hadadi ambaye wakati ule alikuwa kijana alitorokea Misri pamoja na Waedomu wamoja, watumishi wa baba yake. Hadadi na wenzake walisafiri kutoka Midiani, wakawakamata watu wengine kule Parani, wakaenda nao mpaka Misri, kwa mufalme wa Misri. Yeye akamupatia Hadadi nyumba, shamba, na chakula. Hadadi alipata kukubaliwa kabisa mbele ya mufalme wa Misri. Kwa hiyo mufalme wa Misri akamuruhusu shemeki yake, mudogo yake na malkia Tapanesi, aolewe na Hadadi. Huyo dada ya Tapanesi akamuzalia Hadadi mwana aliyeitwa Genubati. Genubati alilelewa na Tapanesi katika nyumba ya mufalme wa Misri, pamoja na wana wa mufalme. Lakini Hadadi aliposikia kule Misri kwamba Daudi na Yoabu jemadari wa waaskari walikuwa wamekufa, alimwambia mufalme wa Misri: “Uniruhusu niondoke nirudi katika inchi yangu.” Lakini mufalme wa Misri akamwuliza: “Nimekunyima nini hata uamue sasa kurudi katika inchi yako?” Naye Hadadi akasema: “Uniache tu niende.” Vilevile, Mungu alimufanya Resoni mwana wa Eliada, akuwe adui ya Solomono. Resoni alikuwa amemutoroka bwana wake, mufalme Hadadezeri wa Zoba. Nyuma ya Daudi kufanya mauaji kule Zoba, Resoni alikusanya watu, naye mwenyewe akakuwa kiongozi wao. Basi, wakaenda Damasiki, wakakaa kule na kumufanya Resoni mufalme wa Damasiki. Resoni alikuwa adui wa Waisraeli siku zote za utawala wa Solomono, akamusumbua sana Solomono kama naye Hadadi alivyomusumbua. Basi, Resoni aliizarau inchi ya Israeli, naye alitawala inchi ya Aramu. Yeroboamu mwana wa Nebati Mwefuraimu wa muji wa Zereda, mutumishi wa Solomono, ambaye mama yake mujane aliitwa Zerua, naye alimwasi mufalme. Kisa cha uasi huo ni hiki: Solomono alijenga uwanja wa Milo na kuimarisha kuta za muji wa baba yake Daudi. Yeroboamu alionekana kuwa kijana hodari na shujaa. Wakati Solomono alipoona kwamba huyo kijana alikuwa mwenye bidii, akamuweka akuwe musimamizi wa kazi za kulazimishwa zilizofanywa na watu wa ukoo wa Yosefu. Siku moja, Yeroboamu alipokuwa akisafiri kutoka Yerusalema, nabii Ahiya wa Shilo alikutana naye katika njia. Ahiya alikuwa akivaa nguo mupya. Wote wawili walikuwa peke yao katikati ya mashamba. Mara moja, Ahiya akavua nguo yake mupya, akaipasua kwa vipande kumi na viwili, halafu akamwambia Yeroboamu: “Ujitwalie vipande kumi maana Yawe, Mungu wa Israeli, anasema: ‘Sasa hivi nitaurarua ufalme na kuuondoa katika mikono ya Solomono, nami nitakupa wewe makabila kumi. Lakini yeye, nitamwachia kabila moja kwa ajili ya mutumishi wangu Daudi, na kwa ajili ya Yerusalema ambao nimeuchagua kuwa wangu katika makabila yote ya Israeli. Nitafanya hivyo kwa sababu Solomono ameniacha, akaabudu miungu ya kigeni: Astaroti mungu wa Wasidoni, Kemosi mungu wa Wamoabu, na Milkomu mungu wa Waamoni. Solomono ameniasi, ametenda maovu mbele yangu. Hakutii masharti yangu na maagizo yangu kama Daudi baba yake alivyofanya. Hata hivyo, sitamunyanganya urizi wote, wala sitamwondolea mamlaka wakati angali anaishi, kwa ajili ya mutumishi wangu Daudi ambaye nilimuchagua, na ambaye alifuata amri zangu na masharti yangu. Lakini, nitamunyanganya mwana wake ufalme ule, nami nitakupatia wewe Yeroboamu makabila kumi. Huyo mwana wa Solomono nitamwachia kabila moja, kusudi wakati wote mutu mumoja wa uzao wa mutumishi wangu Daudi akuwe anatawala Yerusalema, akuwe taa inayoangaza siku zote mbele yangu katika muji ambao nimeuchagua ukuwe pahali pa kuniabudia. Basi, wewe Yeroboamu, nitakufanya kuwa mufalme wa Israeli, nawe utatawala kama unavyopenda. Na kama utashika yote nitakayokuamuru, kama utaishi kulingana na mapenzi yangu, kama utatenda mema mbele yangu kwa kushika masharti yangu na amri zangu, kama vile mutumishi wangu Daudi alivyofanya, mimi nitakuwa pamoja nawe siku zote. Na nitakupatia inchi ya Israeli na kuufanya utawala wako ukuwe imara kama nilivyomufanyia Daudi. Kutokana na hayo, nitawaazibu wazao wa Daudi, lakini si siku zote.’ ” Kwa sababu hiyo, Solomono alijaribu kumwua Yeroboamu. Lakini Yeroboamu akakimbilia Misri kwa Sisaki mufalme wa Misri, akakaa kule mpaka Solomono alipokufa. Mambo mengine ya Solomono, yote aliyofanya na hekima yake yameandikwa katika Kitabu cha Matendo ya Solomono. Kwa muda wa miaka makumi ine, Solomono aliitawala inchi yote ya Israeli, makao yake yakiwa Yerusalema. Kisha, Solomono alikufa, akazikwa katika muji wa baba yake Daudi. Rehoboamu mwana wa Solomono akatawala kwa pahali pake. Basi, Rehoboamu akaenda Sekemu ambako Waisraeli wote walikuwa wamekusanyika kwa kumuweka kuwa mufalme. Naye Yeroboamu mwana wa Nebati alipopata habari juu ya tendo hilo, maana alikuwa angali Misri ambako alikwenda alipomukimbia Solomono, alirudi kutoka Misri. Kisha Waisraeli walituma ujumbe na kumwita. Basi, yeye pamoja na Waisraeli hao wote walimwendea Rehoboamu, wakamwambia: “Baba yako alitubebesha muzigo muzito. Basi, utupunguzie muzigo huo muzito wa baba yako, nasi tutakutumikia.” Naye Rehoboamu akawaambia: “Mwende, murudie kwangu kesho kutwa.” Basi, wakaondoka. Nyuma Rehoboamu alitaka kujua maoni ya wazee ambao walikuwa washauri wa baba yake Solomono alipokuwa angali muzima, akawauliza: “Munanishauria niwape jibu gani watu hawa?” Wazee hao wakamujibu: “Leo ukiwa mutumishi wa watu hawa, ukiwatumikia na kuongea nao vizuri unapowajibu, pale watakuwa watumishi wako siku zote.” Lakini Rehoboamu alizarau shauri la wazee. Pahali pa shauri lile akashauriana na vijana waliokomaa pamoja naye ambao walikuwa washauri wake. Basi, akawauliza: “Ninyi munatoa shauri gani kusudi tuweze kuwajibu watu hawa walioniambia niwapunguzie muzigo ambao baba yangu aliwabebesha?” Hao vijana wakamujibu: “Watu hao waliokuambia baba yako aliwabebesha muzigo muzito, wakakuomba uwapunguzie muzigo ule, wewe uwaambie hivi: ‘Kidole changu kidogo cha mwisho ni kinene zaidi kuliko kiuno cha baba yangu. Muzigo wa baba yangu ulikuwa muzito, lakini wangu utakuwa muzito zaidi. Baba yangu aliwapiga ninyi kwa mijeledi, lakini mimi nitawapiga kwa mijeledi yenye miiba.’ ” Basi, siku ya tatu Yeroboamu pamoja na watu wote wakarudi kwa Rehoboamu kama alivyokuwa amewaagiza. Mufalme akawajibu watu hao kwa ukali, akazarau shauri alilopewa na wazee, akafuata shauri la vijana wenzake, akawaambia: “Baba yangu aliwabebesha muzigo muzito, lakini mimi nitaufanya kuwa muzito zaidi. Baba yangu aliwapiga kwa mijeledi, lakini mimi nitawapiga kwa mijeledi yenye miiba.” Hivyo, mufalme hakuwajali watu kwa sababu jambo hili lilisababishwa na Yawe, kusudi atimize neno lake alilomwambia Yeroboamu mwana wa Nebati, kwa njia ya Ahiya wa Shilo. Lakini watu wote wa Israeli walipoona kwamba mufalme hakuwajali, walimwambia: “Hatuna ushirika wowote na Daudi! Hatuna sehemu yetu kutoka kwa huyo mwana wa Yese. Murudie kwenu, enyi watu wa Israeli! Uitunze nyumba yako mwenyewe, ee Daudi.” Hivyo, watu wa Israeli wakarudi kila mutu kwake. Watu wa Israeli waliokuwa wanakaa katika miji ya Yuda, ndio hao tu waliobaki chini ya utawala wa Rehoboamu. Mufalme Rehoboamu alipomutuma Adoramu, aliyekuwa musimamizi mukubwa wa kazi za kulazimishwa, watu wote wa Israeli walimutupia mawe, wakamwua. Naye Rehoboamu alipanda haraka ndani ya gari lake, akakimbilia Yerusalema. Hivyo watu wa Israeli wakakuwa katika hali ya uasi mbele ya ukoo wa Daudi mpaka leo. Watu wote wa Israeli walipopata habari kwamba Yeroboamu alikuwa amerudi kutoka Misri, walimwita katika mukutano, wakamuweka kuwa mufalme wa Israeli yote. Hakuna kabila lingine lililojiunga na ukoo wa Daudi isipokuwa tu kabila la Yuda. Rehoboamu alipofika Yerusalema, alikusanya waaskari wafundi wa vita elfu mia moja na makumi nane wa makabila ya Yuda na Benjamina, apate kupigana na utawala wa Israeli, kusudi aurudishe utawala kwa Rehoboamu mwana wa Solomono. Lakini ujumbe huu wa Mungu ulitolewa kwa Semaya, mutu wa Mungu: “Umwambie Rehoboamu mwana wa Solomono, mufalme wa Yuda, na watu wote wa kabila la Yuda na Benjamina na watu wengine, kwamba mimi Yawe ninasema hivi: ‘Musiende, wala musipigane na wandugu zenu, watu wa Israeli. Murudie kila mutu kwake, maana hayo yaliyotokea ni mupango wangu.’ ” Basi, wakaufuata ujumbe huu wa Yawe, wakarudi kwao tena kama vile Yawe alivyoagiza. Nyuma ya mambo hayo, mufalme Yeroboamu akaujenga upya muji wa Sekemu kwenye mulima wa Efuraimu. Akakaa kule. Kisha akaenda kujenga muji wa Penueli. Halafu Yeroboamu akaanza kufikirifikiri: “Sasa ufalme utarudi kwa jamaa ya mufalme Daudi kama watu hawa wataendelea kwenda kutoa sadaka katika nyumba ya Yawe kule Yerusalema. Mioyo yao itamugeukia bwana wao Rehoboamu mufalme wa Yuda, nao wataniua mimi.” Basi, kisha kushauriana na wengine, akatengeneza sanamu mbili za zahabu. Kisha akawaambia watu: “Enyi watu wa Israeli, hii ndiyo miungu yenu iliyowatoa katika inchi ya Misri! Hakuna sababu ya kwenda Yerusalema kutoa sadaka kule.” Akaiweka sanamu moja katika muji wa Beteli, na ya pili katika muji wa Dani. Tendo hili likakuwa zambi, maana watu waliandamana kwenda kuzitambikia sanamu hizo kule Beteli na Dani. Vilevile, Yeroboamu alijenga nafasi ya kutambikia juu ya vilima, akachagua makuhani ambao hawakukuwa wa ukoo wa Lawi. Yeroboamu aliamuru vilevile siku ya kumi na tano ya mwezi wa nane ikuwe sikukuu sawa na ile sikukuu iliyokuwa inafanyika kule Yuda. Alitoa sadaka kwenye mazabahu aliyotengeneza kule Beteli mbele ya zile sanamu za wana-ngombe alizozitengeneza, akaweka wale makuhani aliowachagua watumike kila nafasi ya kutolea sadaka aliyotengeneza juu ya vilima. Siku hiyo ya kumi na tano ya mwezi wa nane, aliifanya yeye mwenyewe, naye akaenda Beteli kwa kutambikia. Ndivyo alivyoiimarisha sikukuu hiyo aliyoiweka kwa ajili ya watu wa Israeli, naye mwenyewe akapanda kuiendea mazabahu, kufukiza ubani. Siku moja Yeroboamu alikuwa akisimama pembeni ya mazabahu kusudi afukize ubani. Basi, mutu wa Mungu kutoka Yuda akafika pale Beteli na ujumbe wa Yawe. Mutu huyo akailaani ile mazabahu akisema: “Ee mazabahu, Yawe anasema hivi: ‘Kutazaliwa mutoto katika ukoo wa Daudi, jina lake Yosia. Huyo atawatwaa makuhani wanaotumika kwa nafasi ya ibada na kufukiza ubani juu yako, na kuwatambika juu yako. Hakika, mifupa ya watu itateketezwa juu yako!’ ” Mutu huyo akaonyesha kitambulisho siku ileile, akasema: “Hiki ndicho kitambulisho Yawe alichosema: ‘Mazabahu hii itabomoka, na majivu yanayokuwa juu yake yatamwangika.’ ” Mufalme Yeroboamu aliposikia maneno hayo ya mutu wa Mungu juu ya mazabahu kule Beteli, alinyoosha mukono akasema: “Mumukamate mutu yule!” Na mara moja ule mukono wake aliounyoosha, ukakauka, hakuweza tena kuukunja. Mazabahu nayo ikabomoka, na majivu yake yakamwangika chini, kama kitambulisho kile yule mutu wa Mungu alichokitoa na ujumbe wa Yawe. Basi, mufalme Yeroboamu akamwambia nabii: “Tafazali, umusihi Yawe, Mungu wako, uniombee mukono wangu upate kupona.” Naye nabii akamwomba Yawe, na mukono wa mufalme ukapona, ukarudia kwa hali yake ya zamani. Halafu mufalme akamwambia mutu wa Mungu: “Karibu katika nyumba yangu kula chakula, nami nikupe zawadi.” Lakini mutu wa Mungu akamwambia: “Hata kama ukinipa nusu ya urizi wako, sitakwenda pamoja nawe. Sitakula wala kunywa maji pahali hapa, maana Yawe aliniamuru nisikule chakula au kunywa maji, wala nisirudi kwa njia ileile niliyoifuata kwa kuja hapa.” Basi, mutu yule akaenda zake, wala hakurudi kwa njia ile aliyoifuata kwa kuja Beteli. Wakati ule, kulikuwa nabii mumoja muzee kule Beteli. Wana wake wakamwendea, wakamwelezea mambo yote yule mutu wa Mungu aliyotenda siku hiyo, kule Beteli. Wakamwambia vilevile yale maneno yule mutu aliyomwambia mufalme Yeroboamu. Baba yao akawauliza: “Amefuata njia gani?” Nao wakamwonyesha njia yule mutu wa Mungu aliyoifuata kutoka Yuda. Naye akawaambia watoto wake: “Munitayarishie yule punda.” Nao wakamutayarishia punda, na muzee akapanda juu yake. Akamufuata yule mutu wa Mungu, akamukuta akiikaa chini ya muti wa mwalo. Basi, akamwuliza: “Wewe ndiwe yule mutu wa Mungu kutoka Yuda?” Naye akamujibu: “Ndiyo. Mimi ndiye.” Yule muzee akamwambia: “Karibu katika nyumba yangu, ukule chakula.” Lakini yeye akamwambia: “Siwezi kurudi pamoja nawe, wala kuingia katika nyumba yako. Siwezi kula chakula au kunywa maji pahali hapa, maana, Yawe aliniamuru nisikule chakula au kunywa maji pahali hapa, wala nisirudie kwa njia niliyokuja nayo.” Yule muzee wa Beteli akamwambia: “Mimi vilevile ni nabii kama wewe, na Yawe amesema nami kwa njia ya malaika akisema: ‘Umurudishe kwako, akule chakula na kunywa maji.’ ” Lakini yule nabii muzee alikuwa anamudanganya tu. Basi, mutu wa Mungu akarudi pamoja naye, akakula chakula na kunywa maji kwa huyo muzee. Walipokuwa kwa meza, neno la Yawe lilimufikia yule nabii muzee naye akamwambia kwa sauti yule mutu wa Mungu kutoka Yuda: “Yawe anasema hivi: ‘Wewe umeacha kutii ujumbe wa Yawe. Wewe haukufuata amri Yawe, Mungu wako, aliyokupa. Kwa pahali pake, umerudi hapa, ukakula chakula na kunywa maji pahali hapa ambapo uliambiwa usikule chakula wala kunywa maji. Basi, mwili wako hautazikwa kwenye kaburi la babu zako.’ ” Walipomaliza kula, yule nabii muzee akamutayarishia yule mutu wa Mungu punda, naye akaondoka. Alipokuwa anakwenda zake, simba akakutana naye katika njia, akamwua. Mwili wake ukatupwa pale katika barabara. Punda wake na yule simba wakasimama pembeni yake. Watu waliopitia pale na kuiona maiti katika barabara, na simba akisimama karibu nayo, wakaenda mpaka katika muji yule nabii alimokuwa anakaa, wakawaambia watu. Nabii yule ambaye alikuwa amemukaribisha kwake aliposikia habari hiyo, akasema: “Huyo ni yuleyule mutu wa Mungu aliyekataa kutii neno la Yawe! Yawe amemutuma simba, akamushambulia na kumwua kama alivyokuwa amemwambia.” Hapo akawaambia wana wake: “Munitayarishie punda.” Nao wakamutayarisha. Muzee akaenda, akaikuta maiti ya mutu wa Mungu katika barabara, simba na punda wake pembeni yake. Yule simba hakuikula maiti wala hakumushambulia punda. Basi, yule nabii muzee akaitwaa maiti ya mutu wa Mungu, akaiweka juu ya punda wake, akairudisha Beteli, kuomboleza kifo chake na kumuzika. Basi, akamuzika katika kaburi lake, naye pamoja na wana wake wakaomboleza kifo chake wakisema: “Aa! Ndugu yangu!” Nyuma ya mazishi, nabii huyo akawaambia wana wake: “Nikikufa, munizike katika kaburi hilihili alimozikwa mutu wa Mungu, mifupa yangu pembeni ya mifupa yake. Mambo yote aliyoagizwa na Yawe juu ya mazabahu ya Beteli, na nafasi yote ya kutambikia juu ya vilima vya Samaria, hakika yatatimia.” Yeroboamu hakuuacha upotovu wake; aliendelea kuchagua watu wa kawaida kuwa makuhani, watumike kwa nafasi ya kutambikia juu ya vilima. Mutu yeyote aliyejitolea, alimutakasa kuwa kuhani wa nafasi ya kutambikia kule juu ya vilima. Tendo hili likakuwa zambi ambayo ilisababisha ukoo wa Yeroboamu ufutiliwe mbali na kuangamizwa. Wakati ule, Abiya mwana wa mufalme Yeroboamu, akagonjwa. Yeroboamu akamwambia muke wake: “Ujigeuze kusudi watu wasitambue kwamba wewe ni muke wangu, uende Shilo kwa nabii Ahiya aliyesema kwamba mimi nitakuwa mufalme wa Israeli. Umupelekee mikate kumi, na maandazi, na chupa moja ya asali. Yeye atakuambia yatakayomupata mutoto wetu.” Basi, muke wa Yeroboamu akaondoka, akaenda Shilo kwa Ahiya. Wakati ule, Ahiya alikuwa hawezi tena kuona sawasawa kwa sababu ya uzee. Yawe alikuwa amekwisha kumwambia Ahiya kwamba muke wa Yeroboamu alikuwa katika njia, anakuja kumwuliza yatakayomupata mwana wake mugonjwa, na jinsi atakavyomujibu. Muke wa Yeroboamu alipofika, alijisingizia kuwa mutu mwingine. Lakini Ahiya alipomusikia anaingia kwenye mulango, alisema: “Karibu ndani muke wa Yeroboamu. Lakini mbona unajigeuza kuwa mutu mwingine? Niko na ujumbe usiokuwa muzuri kwako! Kwenda umwambie Yeroboamu kwamba Yawe, Mungu wa Israeli, anasema hivi: ‘Nilikuchagua kati ya watu, nikakufanya kiongozi wa watu wangu Waisraeli, nikaunyanganya ufalme utoke kwa wazao wa Daudi, nikakupa wewe. Lakini wewe ni kinyume kabisa cha mutumishi wangu Daudi ambaye alizishika amri zangu. Alifuata mapenzi yangu kwa moyo wake wote na kutenda tu yanayokuwa sawa mbele ya macho yangu. Wewe umetenda uovu mubaya zaidi kuliko waliotenda wale waliokutangulia. Wewe umenikasirikisha kwa kujitengenezea miungu mingine na sanamu za kufua, kisha umeniacha. Basi, sasa nitailetea jamaa hii ya Yeroboamu hasara, nitawaua wanaume wote wa jamaa yake katika Israeli, akuwe mutumwa au huru. Watu wa jamaa yake wote nitawateketeza kama vile mutu anavyoteketeza mavi, mpaka yatoweke. Mutu yeyote wa jamaa ya Yeroboamu atakayekufia katika muji, imbwa watamukula; na yeyote atakayekufia katika shamba, ndege watamukula.’ Yawe amesema hivyo.” Ahiya akamwambia muke wa Yeroboamu: “Simama, urudie kwako sasa. Mara tu utakapoingia katika muji, mwana wako atakufa. Watu wote wa Israeli watafanya kilio na kumuzika. Lakini, ni huyo tu wa jamaa ya Yeroboamu atakayezikwa, maana ni yeye tu wa jamaa ya Yeroboamu aliyepata kupendezwa na Yawe, Mungu wa Israeli. Tena leo hii, Yawe ataweka mufalme mwingine katika Israeli ambaye ataua watu wa jamaa ya Yeroboamu. Hakika, tangu sasa, Yawe atawapiga watu wa Israeli, nao watatikisika kama unyasi unavyotikiswa ndani ya muto. Atawaongoa kutoka inchi hii nzuri aliyowapa babu zao, na kuwatawanya mbali, ngambo ya muto Furati, kwa sababu wamemukasirikisha Yawe kwa kujitengenezea sanamu za Ashera. Yawe ataitupilia Israeli kwa sababu ya zambi za Yeroboamu ambaye alitenda zambi na kuwasukuma watu wa Israeli vilevile watende zambi.” Halafu, muke wa Yeroboamu akaondoka, akashika safari mpaka Tirza. Mara tu alipofika kwenye mulango, mutoto akakufa. Watu wote wa Israeli wakamuzika na kufanya kilio kama vile Yawe alivyosema, kwa njia ya nabii Ahiya, mutumishi wake. Matendo mengine ya mufalme Yeroboamu, jinsi alivyopigana vita na alivyotawala, yote yameandikwa katika Kitabu cha Mambo ya Siku za Wafalme wa Israeli. Yeroboamu alitawala kwa muda wa miaka makumi mbili na mbili, halafu akakufa, na mwana wake Nadabu akatawala kwa pahali pake. Rehoboamu mwana wa Solomono alikuwa na umri wa miaka makumi ine na mumoja alipoanza kutawala inchi ya Yuda. Naye alitawala kwa muda wa miaka kumi na saba katika Yerusalema, muji ambao Yawe aliuchagua kati ya miji ya makabila yote ya Israeli kusudi aabudiwe humo. Mama ya Rehoboamu jina lake lilikuwa Nama kutoka kabila la Waamoni. Watu wa Yuda walitenda maovu mbele ya Yawe. Walimukasirikisha kwa zambi zao walizotenda, nyingi kuliko za babu zao. Walijitengenezea vilevile pahali pa ibada, minara ya kutambikia, na sanamu za Ashera, juu ya kila kilima kirefu na chini ya kila muti wenye majani mengi. Kukakuwa hata ibada za uasherati katika inchi, nao walitenda matendo ya kuchukiza, sawasawa na yale matendo ya mataifa ambayo Mungu aliyafukuza mbele ya Waisraeli. Katika mwaka wa tano wa utawala wa Rehoboamu, Sisaki mufalme wa Misri aliushambulia Yerusalema. Akaitwaa hazina yote ya nyumba ya Yawe na ya nyumba ya kifalme. Alitwaa kila kitu; naye alitwaa ngao zote za zahabu Solomono alizozitengeneza. Pahali pa ngao hizo, mufalme Rehoboamu alitengeneza ngao za shaba na kuziweka chini ya ulinzi wa wachungaji wa mulango wa nyumba ya kifalme. Kila wakati mufalme alipokwenda katika nyumba ya Yawe, walinzi walizibeba ngao hizo, na nyuma walizirudisha katika chumba cha ulinzi. Mambo mengine ya Rehoboamu na yote aliyofanya yameandikwa katika Kitabu cha Mambo ya Siku za Wafalme wa Yuda. Siku zote kulikuwa vita kati ya Rehoboamu na Yeroboamu. Nyuma, Rehoboamu alikufa na kuzikwa kwenye makaburi ya wazee wake, katika muji wa Daudi. Mama yake aliitwa Nama kutoka katika kabila la Waamoni, na mwana wake Abiyamu akatawala kwa pahali pake. Abiyamu alianza kutawala kule Yuda katika mwaka wa kumi na nane wa utawala wa mufalme Yeroboamu mwana wa Nebati. Alitawala kwa muda wa miaka mitatu akiwa Yerusalema. Mama yake, ambaye alikuwa binti ya Abisaloma, aliitwa Maka. Abiyamu alitenda zambi zilezile baba yake alizotenda, wala hakukuwa na moyo mwaminifu kwa Yawe, Mungu wake, kama babu yake Daudi alivyokuwa. Hata hivyo, kwa ajili ya Daudi, Yawe alimupatia Abiyamu mwana atakayetawala nyuma yake, kuwa taa ya kuangaza Yerusalema na kuuweka imara Yerusalema. Yawe alifanya hivyo kwa sababu Daudi alitenda mema mbele yake na hakuenda pembeni ya maagizo ya Yawe siku za maisha yake yote, isipokuwa tu lile jambo la Uria Muhiti. Kulikuwa vita kati ya Rehoboamu na Yeroboamu wakati wote alipokuwa mutawala. Matendo mengine ya Abiyamu na yote aliyofanya yameandikwa katika Kitabu cha Mambo ya Siku za Wafalme wa Yuda. Abiyamu na Yeroboamu waliishi katika hali ya vita. Kwa mwisho, Abiyamu akakufa na kuzikwa katika muji wa Daudi na mwana wake Asa akatawala pahali pake. Katika mwaka wa makumi mbili wa utawala wa Yeroboamu mufalme wa Israeli, Asa alianza kutawala kule Yuda. Alitawala kwa muda wa miaka makumi ine na mumoja. Tate yake aliitwa Maka, binti ya Abisaloma. Mufalme Asa alitenda mambo yanayokuwa mema mbele ya Yawe kama vile Daudi babu yake alivyofanya. Aliwafukuza toka katika inchi wale wote waasherati wa kidini, akaziondoa sanamu zote ambazo babu zake walikuwa wamezitengeneza. Akamwondoa tate yake Maka cheo chake cha mama malkia, kwa sababu alitengeneza sanamu ya Ashera na hiyo sanamu akaivunjavunja na kuiteketeza kwenye bonde la Kidroni. Lakini nafasi ya kutambikia miungu juu ya vilima haikuharibiwa. Hata hivyo, yeye alikuwa na moyo mwaminifu kwa Yawe maisha yake yote. Alirudisha katika nyumba ya Yawe matoleo yaliyokuwa yametakaswa na baba yake, pamoja na yale yake yeye mwenyewe: vyombo vya feza, zahabu na vyombo vingine vyote. Mufalme Asa wa Yuda na mufalme Basha wa Israeli walikuwa na vita kati yao wakati wote walipokuwa wakitawala. Basha, mufalme wa Israeli, aliishambulia inchi ya Yuda na kuanza kuujenga muji wa Rama kusudi apate kuzuia mutu yeyote asitoke wala asiingie kwa Asa, mufalme wa Yuda. Halafu mufalme Asa akatwaa feza na zahabu yote iliyobaki katika hazina ya nyumba ya Yawe na katika hazina ya nyumba ya kifalme, akawapa watumishi wake, akawatuma Damasiki kwa Beni-Hadadi mwana wa Taburimoni, mujukuu wa Hesioni, mufalme wa Aramu, akasema: “Tufanye mapatano ya ushirikiano kati yangu na wewe kama vile baba yangu na baba yako walivyofanya. Angalia, nimekutumia zawadi ya feza na zahabu; kwenda uvunje mapatano ya ushirikiano unaokuwa kati yako na mufalme Basha wa Israeli, kusudi aache mashambulizi juu yangu.” Hapo mufalme Beni-Hadadi akakubaliana na mufalme Asa, akawatuma majemadari wake na waaskari wake kwenda kuishambulia miji ya Israeli. Nao wakateka miji Iyoni, Dani, Abeli-Beti-Maka, Kineroti yote, na inchi yote ya Nafutali. Mufalme Basha alipopata habari za mashambulizi hayo aliacha kuujenga muji wa Rama akaenda kukaa Tirza. Halafu mufalme Asa akatoa tangazo kwa watu wote wa Yuda, bila kumwacha hata mutu mumoja, wahamishe mawe ya Rama na mbao, vifaa ambavyo Basha alivitumia kwa kujenga. Kisha mufalme Asa alitumia vifaa hivyo kwa kujenga kuta za Geba, katika inchi ya Benjamina na Misipa. Matendo mengine yote ya Asa, ushujaa wake na miji yote aliyoijenga, yote yameandikwa katika Kitabu cha Mambo ya Siku za Wafalme wa Yuda. Wakati wa uzee wake, Asa alishikwa na ugonjwa wa miguu. Kisha, Asa akakufa, akazikwa katika makaburi ya kifalme, katika muji wa Daudi, naye mwana wake Yehosafati akatawala kwa pahali pake. Katika mwaka wa pili wa utawala wa Asa kule Yuda, Nadabu mwana wa Yeroboamu alianza kutawala katika inchi ya Israeli. Alitawala kwa muda wa miaka miwili. Nadabu alitenda maovu mbele ya Yawe; alifuata mwenendo wa baba yake na kutenda zambi ileile ambayo aliwasukuma watu wa Israeli watende. Basha mwana wa Ahiya, wa kabila la Isakari, akamufanyia Nadabu shauri baya. Basi, wakati Nadabu na waaskari wake walipokuwa wakiushambulia muji wa Gibetoni wa Wafilistini, Basha akamwua, akatawala kwa pahali pake. Huo ulikuwa mwaka wa tatu wa utawala wa mufalme Asa wa Yuda. Mara tu alipoanza kutawala, Basha akawaua watu wote wa jamaa ya Yeroboamu; hakuacha muzima hata mutu mumoja wa jamaa ya Yeroboamu. Hiyo ilikuwa sawa na yale Yawe aliyosema kwa njia ya mutumishi wake Ahiya wa Shilo. Mambo haya yalifanyika kwa sababu Yeroboamu alimukasirikisha Yawe, Mungu wa Israeli, kwa zambi yake na kwa kuwasukuma watu wa Israeli watende zambi. Mambo mengine ya Nadabu na yote aliyofanya yameandikwa katika Kitabu cha Mambo ya Siku za Wafalme wa Israeli. Mufalme Asa wa Yuda na mufalme Basha wa Israeli walikuwa na vita kati yao wakati wote walipokuwa wakitawala. Katika mwaka wa tatu wa utawala wa Asa mufalme wa Yuda, Basha mwana wa Ahiya, alianza kutawala Israeli kutoka Tirza. Alitawala kwa muda wa miaka makumi mbili na mine. Basha alitenda maovu mbele ya Yawe; alifuata mwenendo wa Yeroboamu na kutenda zambi ileile ambayo aliwasukuma watu wa Israeli watende. Neno la Yawe lilimufikia Yehu mwana wa Hanani kusema hivi juu ya Basha: “Wewe Basha, mimi nilikuinua kutoka katika mavumbi, nikakufanya kiongozi wa watu wangu Waisraeli. Wewe umefuata mwenendo wa Yeroboamu. Uliwasukuma watu wangu Waisraeli watende zambi na kunikasirikisha kwa zambi zao. Sasa, nitakufagia kabisa wewe na jamaa yako. Nitaitendea jamaa yako kama vile nilivyoitendea jamaa ya Yeroboamu mwana wa Nebati. Mutu yeyote wa jamaa yako atakayekufia ndani ya muji, imbwa watamukula; na mutu yeyote atakayekufia katika shamba, ndege watamukula.” Matendo mengine ya Basha na ushujaa wake, yote yameandikwa katika Kitabu cha Mambo ya Siku za Wafalme wa Israeli. Nyuma ya hayo, Basha akakufa, akazikwa kule Tirza; mwana wake Ela akatawala kwa pahali pake. Tena, neno la Yawe lilifika kwa njia ya nabii Yehu mwana wa Hanani juu ya Basha na jamaa yake, kwa sababu ya maovu aliyotenda mbele ya Yawe. Basha alimukasirikisha Yawe kwa matendo yake; alimwiga Yeroboamu na jamaa yake na kuiletea jamaa yake maangamizi. Katika mwaka wa makumi mbili na sita wa utawala wa Asa mufalme wa Yuda, Ela mwana wa Basha alianza kutawala kule Israeli akiwa Tirza. Alitawala kwa muda wa miaka miwili. Jemadari wake Simuri ambaye alisimamia nusu ya kundi ya magari yake ya vita alimwasi. Siku moja, mufalme Ela alipokuwa kule Tirza katika nyumba ya Arsa aliyekuwa musimamizi wa nyumba ya kifalme, alikunywa, akalewa. Basi, Simuri akaingia ndani, akamwua. Kisha akatawala kwa pahali pake. Huu ulikuwa mwaka wa makumi mbili na saba wa utawala wa Asa mufalme wa Yuda. Mara tu alipoanza kutawala, Simuri aliwaua watu wote wa jamaa ya Basha. Hakumwacha hata mwanaume mumoja wa jamaa yake wala warafiki zake. Ilikuwa kama Yawe alivyosema juu ya Basha, kwa njia ya nabii Yehu. Mambo haya yalifanyika kwa sababu ya zambi Basha na mwana wake Ela alizotenda. Walimukasirikisha Yawe, Mungu wa Israeli, kwa kutenda zambi na kuwasukuma watu wa Israeli watende zambi kwa sanamu za miungu yao. Mambo mengine ya Ela na yote aliyofanya yameandikwa katika Kitabu cha Mambo ya Siku za Wafalme wa Israeli. Simuri alitawala kule Israeli akiwa Tirza kwa muda wa siku saba. Huo ulikuwa mwaka wa makumi mbili na saba wa utawala wa Asa mufalme wa Yuda. Watu wa Israeli walikuwa wamepiga kambi kwa kushambulia muji wa Gibetoni wa Wafilistini. Wakati waaskari wa Israeli waliposikia kwamba Simuri aliasi na kumwua mufalme, wote wakamuweka Omuri, jemadari wa waaskari wao, kuwa mufalme wa Israeli siku ileile. Omuri na waaskari wake wakaondoka Gibetoni, wakaenda na kuushambulia muji wa Tirza. Simuri alipoona kwamba muji umekamatwa, akaingia katika munara, ndani ya nyumba ya kifalme, akaichoma kwa moto, naye akakufia mule. Jambo hilo lilifanyika kwa sababu ya zambi alizotenda. Alitenda maovu mbele ya Yawe; alifuata mwenendo wa Yeroboamu na kuwasukuma watu wa Israeli watende zambi. Matendo mengine ya Simuri na uasi wake, yote yameandikwa katika Kitabu cha Mambo ya Siku za Wafalme wa Israeli. Sasa, watu wa Israeli waligawanyika kwa makundi mawili: kundi moja lilimutambua Tibuni mwana wa Ginati kuwa mufalme, na kundi la pili lilimutambua Omuri. Watu wa kundi lililomutambua Omuri, wakawazidia nguvu wale waliomutambua Tibuni mwana wa Ginati. Tibuni akakufa na Omuri akakuwa mufalme. Omuri alianza kutawala katika mwaka wa makumi tatu na mumoja wa utawala wa Asa mufalme wa Yuda. Alitawala kwa muda wa miaka kumi na miwili. Miaka sita alikuwa anatawala akiwa katika muji wa Tirza. Alinunua mulima wa Samaria kwa vikoroti elfu sita vya feza kutoka kwa mutu mumoja anayeitwa Semeri, akajenga muji wenye kuta juu yake. Muji wenyewe akauita Samaria, kwa heshima ya Semeri aliyekuwa mwenyeji wa mulima huo hapo zamani. Omuri alitenda maovu mbele ya Yawe. Alitenda maovu zaidi ya wale wote waliomutangulia. Alifuata mwenendo wa Yeroboamu mwana wa Nebati na kutenda zambi ambazo aliwasukuma watu wa Israeli watende. Akamukasirikisha Yawe, Mungu wa Israeli, juu ya kuabudu sanamu za miungu. Matendo mengine ya Omuri na ushujaa wake, yote yameandikwa katika Kitabu cha Mambo ya Siku za Wafalme wa Israeli. Nyuma ya hayo, Omuri akakufa, akazikwa kule Samaria. Mwana wake Ahabu akatawala kwa pahali pake. Katika mwaka wa makumi tatu na nane wa utawala wa Asa mufalme wa Yuda, Ahabu mwana wa Omuri alianza kutawala katika inchi ya Israeli. Alitawala kule Samaria kwa muda wa miaka makumi mbili na mbili. Ahabu alitenda maovu mbele ya Yawe kuliko wafalme wote waliomutangulia. Tena, zaidi ya kufuata mwenendo mubaya wa Yeroboamu mwana wa Nebati, Ahabu alimwoa Yezebeli binti ya Etibali mufalme wa Wasidoni. Akamutumikia na kumwabudu Bali. Alimujengea Bali hekalu kule Samaria, na ndani yake akatengeneza mazabahu ya kumutambikia. Vilevile, alitengeneza sanamu ya Ashera. Ahabu alitenda maovu mengi, akamukasirikisha Yawe Mungu wa Israeli zaidi ya wafalme wote wa Israeli waliomutangulia. Wakati wa utawala wake, Hieli wa muji wa Beteli aliujenga upya muji wa Yeriko. Na sawa kabisa na neno Yawe alilosema kwa njia ya Yoshua mwana wa Nuni, Hieli alikufiwa na muzaliwa wake wa kwanza aliyeitwa Abiramu, wakati wa kuiweka misingi ya Yeriko. Akakufiwa vilevile na mwana wake mudogo aliyeitwa Segubu, wakati wa kuweka milango ya muji wa Yeriko. Basi Elia wa kijiji cha Tisibe katika jimbo la Gileadi akamwambia mufalme Ahabu: “Kama vile Yawe, Mungu wa Israeli, ambaye ninamutumikia, anavyoishi, hakutakuwa umande wala mvua mpaka nitakapotoa amri.” Kisha, neno la Yawe lilimufikia Elia kusema hivi: “Ondoka hapa uelekee upande wa mashariki, ujifiche kwenye kijito cha Keriti kinachokuwa upande wa mashariki wa muto Yordani. Kule, utapata maji ya kunywa katika kijito kile. Tena nimewaamuru vibombobombo wakuletee chakula.” Basi, Elia akatii agizo la Yawe, akaenda kukaa kwenye kijito cha Keriti kinachokuwa upande wa mashariki wa muto Yordani. Vibombobombo wakakuwa wanamuletea mukate na nyama, asubui na magaribi; akapata na maji ya kunywa katika kijito kile. Lakini, nyuma ya siku chache kijito kikakauka kwa sababu hakukunyesha mvua katika inchi. Hapo, neno la Yawe lilimufikia Elia kusema hivi: “Ondoka uende katika muji wa Zerepata, karibu na Sidona, ukae kule. Nimemwamuru mujane mumoja akupatie chakula kule.” Basi, Elia akaondoka, akaenda Zerepata. Alipofika kwenye mulango wa muji, akamukuta mwanamuke mumoja mujane akiokota kuni. Elia akamwita mwanamuke huyo na kumwambia: “Uniletee maji nikunywe.” Yule mwanamuke alipokuwa anaondoka, Elia akamwita tena na kumwambia: “Uniletee na kipande cha mukate vilevile.” Huyo mwanamuke akamwambia: “Kama vile Yawe Mungu wako anavyoishi, sina mukate hata kidogo. Niko tu na unga unaoweza kujaa mukono mumoja katika chungu na mafuta kidogo katika chupa. Nimefika hapa kuokota kuni, kisha niende kwangu kupika chakula hicho, mwana wangu na mimi tukule, kisha tungojee kufa.” Elia akamwambia: “Usiogope. Kwenda ufanye kama vile ulivyosema. Lakini unitengenezee mimi kwanza na kuniletea andazi dogo, kisha ujitengenezee wewe na mwana wako chakula. Maana, Yawe, Mungu wa Israeli, anasema hivi: ‘Unga unaokuwa ndani ya chungu chako hautapunguka wala mafuta yanayokuwa ndani ya chupa hayatakwisha, mpaka pale mimi Yawe nitakaponyesha mvua katika inchi.’ ” Basi, yule mwanamuke mujane akaenda akafanya kama vile alivyoambiwa na Elia hata mama huyo, jamaa yake na Elia wakapata chakula kwa siku nyingi. Unga ndani ya chungu haukupunguka, wala mafuta katika chupa hayakuisha sawa kabisa na neno la Yawe alilomwambia Elia aseme. Nyuma ya hayo, mwana wa mwanamuke huyo mwenye nyumba akagonjwa, na hali yake ikazidi kuwa mbaya, hata kwa mwisho akakufa. Yule mwanamuke akamwambia Elia: “Ewe mutu wa Mungu, kuna maneno gani kati yako nami? Kumbe ulikuja kwangu kwa kuzifichua zambi zangu na kusababisha kifo cha mwana wangu?” Elia akamwambia: “Unipe mwana wako.” Basi, Elia akamutwaa mutoto toka kifua cha mama yake, akamupeleka juu katika chumba chake, akamulalisha juu ya kitanda chake. Kisha akamusihi Yawe akisema: “Ee Yawe, Mungu wangu, hata mwanamuke huyu mujane ambaye ninakaa kwake, naye ananitunza, unamuletea hasara kwa kumwua mwana wake?” Kisha Elia akajinyoosha juu ya mutoto yule mara tatu na kumwomba Yawe: “Ee Yawe, Mungu wangu, umurudishie mutoto huyu roho yake!” Yawe akasikiliza ombi la Elia. Mutoto akaanza kupumua tena. Elia akamurudisha mutoto chini kwa mama yake, akamwambia: “Angalia! Mwana wako yuko muzima.” Huyo mwanamuke mujane akamwambia Elia: “Sasa ninajua kwa hakika kwamba wewe ni mutu wa Mungu, na maneno Yawe aliyokupa uyaseme ni ya kweli.” Nyuma ya siku nyingi, katika mwaka wa tatu wa ukosefu wa mvua, neno la Yawe lilimufikia Elia kusema hivi: “Kwenda ujionyeshe kwa mufalme Ahabu, halafu nitanyesha mvua katika inchi.” Basi, Elia akaenda kujionyesha kwa Ahabu. Wakati huo, njaa ilikuwa kali sana kule Samaria. Basi, Ahabu akamwita Obadia musimamizi wa nyumba ya kifalme. Obadia alikuwa mutu anayemwogopa Yawe sana, na wakati Yezebeli alipowaua manabii wa Yawe, Obadia aliwachukua manabii mia moja, akawaficha makumi tano tano ndani ya pango, akakuwa anawapelekea chakula na maji. Ahabu akamwambia Obadia: “Labda tutapata majani na pale tutaokoa farasi na nyumbu wetu wamoja.” Basi, wakagawanyana inchi kusudi wapate kuichunguza yote. Ahabu akaenda upande mumoja na Obadia upande mwingine. Obadia alipokuwa katika njia, alikutana na Elia; naye Obadia alipomutambua Elia, aliinama chini na kusema: “Hakika, ni wewe bwana wangu Elia?” Elia akamwambia: “Ndiyo! Ni mimi Elia. Kwenda umwambie bwana wako kwamba niko hapa.” Obadia akasema: “Nimefanya kosa gani hata utake kunitia katika hatari kusudi niuawe na mufalme Ahabu? Ninakuapia kwa jina la Yawe, Mungu wako, Mwenye Uzima, kwamba mufalme amekuwa akikutafuta katika dunia yote. Na mufalme yeyote akisema kwamba haujaonekana kule, Ahabu alimutaka huyo mufalme aape na watu wake kwamba kweli hauko. Na sasa, unataka niende kumwambia kwamba wewe uko hapa! Ninaogopa kwamba mara tu nitakapoondoka, Roho wa Yawe atakunyanyua na kukupeleka pahali nisipopajua! Nikienda kumwambia Ahabu kwamba uko hapa, naye akikutafuta na asikupate, ataniua mimi, ingawa mimi mutumishi wako ninamwogopa Yawe tangu ujana wangu. Hauna habari kwamba Yezebeli alipokuwa akiwaua manabii wa Yawe, mimi niliwatwaa manabii mia moja nikawaficha makumi tano tano katika pango, nikakuwa ninawapatia chakula na maji? Sasa unaniambia niende kumwambia bwana wangu kwamba wewe Elia uko hapa! Ahabu ataniua.” Elia akamwambia: “Kama vile Yawe wa majeshi anavyoishi, yule ambaye ninamutumikia: leo hii nitajitokeza mbele ya mufalme.” Basi, Obadia akaenda kwa mufalme Ahabu, akamupa habari hizo. Naye Ahabu akaenda kukutana na Elia. Ahabu alipomwona Elia, alisema: “Hakika ni wewe unayetaabisha Waisraeli?” Elia akamujibu: “Mwenye kutaabisha Waisraeli si mimi, lakini ni wewe na jamaa ya baba yako. Ninyi mumepita pembeni ya amri za Yawe na kuabudu Bali. Sasa, uwakusanye watu wote wa Israeli mbele yangu kule kwenye mulima Karmeli. Vilevile, uwakusanye wale manabii mia ine na makumi tano wa Bali, na manabii mia ine wa Ashera ambao wanakulishwa na malkia Yezebeli.” Basi, Ahabu akawaita watu wote wa Israeli, akawakusanya na manabii wote kule kwenye mulima Karmeli. Kisha, Elia akawakaribia watu hao, akawaambia: “Mutaendelea kusitasita ndani ya mioyo mpaka wakati gani? Ikiwa Yawe ni Mungu, mumufuate; lakini ikiwa Bali ni Mungu, basi, mumufuate.” Lakini watu hawakumujibu neno lolote. Halafu, Elia akawaambia: “Mimi peke yangu tu ndiye nabii wa Yawe niliyebaki, lakini manabii wa Bali wapo mia ine na makumi tano. Basi! Mulete ngombe dume wawili. Manabii wa Bali wajichagulie ngombe dume mumoja, wamuchinje, wamukate vipandevipande na kumuweka juu ya kuni, bila kuwasha moto. Nami vilevile nitamutwaa yule ngombe dume mwingine, nitamuchinja na kumuweka juu ya kuni bila kuwasha moto. Kisha, wao watamwomba mungu wao, nami nitamwomba Yawe. Mungu atakayejibu kwa kuleta moto, yule ndiye Mungu wa kweli.” Na pale watu wote wakasema: “Sawa!” Kisha, Elia akawaambia manabii wa Bali: “Ninyi ni wengi. Basi, muanze. Mujichagulie, mutayarishe ngombe dume, mumutayarishe na kumwomba mungu wenu, lakini musiwashe moto.” Hao manabii wakamutwaa ngombe dume wao waliyepewa, wakamutayarisha, kisha wakaanza kumulilia Bali kutokea asubui mpaka saa sita za muchana, wakirukaruka pembeni ya mazabahu waliyotengeneza wakisema: “Ee Bali, utusikilize!” Lakini hakukutokea sauti yoyote, wala hakuna aliyewajibu. Ilipofika saa sita muchana, Elia akaanza kuwachekelea akisema: “Muombe kwa sauti kubwa zaidi! Yeye ni mungu, labda iko na kazi nyingi au ametoka na kusafiri! Labda analala, munapaswa kumwamusha!” Manabii hao wakapiga kelele zaidi, wakajikatakata kwa visu na wembe, kufuatana na desturi yao, hata damu ikawatiririka. Wakaendelea kupiga makelele na kufanya kama vile wenda-wazimu mpaka nyuma ya saa sita wakati wa kutoa sadaka. Lakini hakuna aliyewajibu wala kuwajali. Basi, Elia akawaambia watu: “Musogee karibu nami.” Wao wakamukaribia. Kisha Elia akaijenga upya mazabahu ya Yawe iliyokuwa imebomolewa. Alitwaa mawe kumi na mawili, hesabu ya makabila kumi na mawili yaliyopewa majina ya wana wa Yakobo ambaye neno la Yawe lilimufikia kusema hivi: “Jina lako litakuwa Israeli.” Kwa mawe hayo, Elia alimujengea Yawe mazabahu. Akachimba mufereji pembenipembeni ya mazabahu hiyo, mufereji ambao unaweza kujazwa na maji yapata litre kumi na ine. Kisha akapanga kuni vizuri, akakata vipandevipande ile ngombe dume, akaviweka juu ya kuni. Kisha akawaambia watu: “Mujaze mitungi mine maji muimwangie juu ya sadaka hii ya kuteketezwa pamoja na kuni.” Wakafanya hivyo. Kisha akawaambia: “Mufanye hivyo tena.” Nao wakafanya hivyo kwa mara ya pili. Naye akawaambia: “Mufanye hivyo tena kwa mara ya tatu.” Nao wakafanya hivyo. Maji yakatiririka chini pande zote za mazabahu, hata yakajaa ndani ya mufereji. Kwa wakati wa kutoa sadaka ya magaribi, nabii Elia aliikaribia mazabahu, akaomba: “Ee Yawe, Mungu wa Abrahamu, Isaka na Yakobo, uwaonyeshe watu leo hii kwamba wewe ndiwe Mungu wa Israeli, na kwamba mimi ni mutumishi wako na nimefanya mambo haya kwa amri yako. Unijibu, ee Yawe, unijibu kusudi watu hawa wajue kwamba wewe Yawe ndiwe Mungu, na kwamba umeigeuza mioyo yao wakurudilie.” Mara moja, Yawe akashusha moto, ukaiteketeza sadaka ile ya kuteketezwa, kuni, mawe na mavumbi, na kuyakausha maji yote katika mufereji. Watu walipoona hivyo, walianguka uso mpaka chini na kusema: “Yawe ndiye Mungu! Yawe ndiye Mungu!” Halafu Elia akawaambia: “Muwakamate manabii wote wa Bali. Musimwache hata mumoja wao atoroke!” Basi, watu wakawakamata wote, naye Elia akawapeleka kwenye muto Kisoni, akawauia kule. Nyuma ya hayo, Elia akamwambia mufalme Ahabu: “Kwenda kula na kunywa. Ninasikia kishindo cha mvua.” Basi, Ahabu akaenda zake kula na kunywa. Naye Elia akapanda juu ya kilele cha mulima Karmeli, na kule akainama uso mpaka chini na kuuweka uso wake katikati ya magoti yake. Kisha akamwambia mutumishi wake: “Sasa, kwenda uangalie kwa upande wa bahari.” Mutumishi akaenda, akaangalia, kisha akarudia akasema: “Hakuna kitu.” Elia akamwambia: “Kwenda tena mara saba.” Kwa mara ya saba, yule mutumishi akarudia, akasema: “Ninaona wingu dogo kama mukono wa mutu linatoka katika bahari.” Elia akamwambia: “Kwenda umwambie mufalme Ahabu atayarishe gari lake la vita, ateremuke, asipate kuzuiliwa na mvua.” Nyuma ya wakati kidogo mbingu zikatanda mawingu mazito, upepo ukavuma, kukanyesha mvua kubwa. Ahabu naye akapanda ndani ya gari lake la vita, akarudia Yezereheli. Nguvu ya Yawe ikamufikia Elia, naye akajitayarisha kusafiri, akakimbia na kumutangulia Ahabu kuingia ndani ya muji Yezereheli. Mufalme Ahabu alimwelezea muke wake Yezebeli mambo yote Elia aliyofanya na jinsi alivyowaua manabii wa Bali kwa upanga. Yezebeli akatuma mujumbe kwa Elia amwambie: “Miungu waniue, ninakuapia, kama kesho nisipokuua kwa wakati kama huu sawa vile ulivyowaua wale manabii.” Elia akakimbilia katika muji wa Beri-Seba katika jimbo la Yuda, kule alikomwacha mutumishi wake, naye akatembea mwendo wa siku nzima kuingia katika jangwa. Basi, akafika, akaikaa chini ya muti mumoja wa muretemu. Halafu, akaomba apate kufa, akisema: “Inatosha! Siwezi tena. Ee Yawe, sasa utoe uzima wangu. Mimi si bora kuliko babu zangu.” Basi, Elia akalala chini ya muti ule, akashikwa na usingizi. Kisha muda kidogo, malaika akakuja, akamugusa na kumwambia: “Amuka ukule.” Elia alipoangalia, akaona mukate uliokaangwa juu ya makaa, na chupa ya maji karibu na kichwa chake. Basi, akakula, akakunywa na akalala tena. Malaika wa Yawe akamufikia tena kwa mara ya pili, akamugusa na kumwambia: “Amuka ukule, kama sivyo safari itakuwa ngumu sana kwako.” Elia akaamuka, akakula na kunywa. Kisha akatembea kwa nguvu ya chakula hicho mwendo wa siku makumi ine, muchana na usiku, mpaka Horebu kwenye mulima wa Mungu. Kule, akafika kwenye pango, akakaa mule. Mara moja Yawe akamutolea ujumbe: “Elia! Unafanya nini hapa?” Naye akasema: “Ninaona uchungu na wivu, ee Yawe, Mungu wa majeshi, kwa sababu watu wa Israeli wamevunja agano lako, wakazibomoa mazabahu zako na kuwaua manabii wako kwa upanga; ni mimi tu niliyebaki, nami vilevile wananiwinda waniue!” Yawe akamwambia: “Kwenda usimame juu ya mulima, mbele yangu mimi Yawe.” Basi, Yawe akapita na kuuvumisha upepo mukali ambao uliporomosha milima na kuvunja mawe makubwa. Lakini Yawe hakukuwa katika upepo ule. Upepo ukapita, kukakuwa tetemeko la inchi. Lakini Yawe hakukuwa katika tetemeko la inchi. Tetemeko likapita, kukakuwa moto. Lakini Yawe hakukuwa katika moto ule. Nyuma ya moto, kukatokea sauti ndogo, tulivu. Basi, Elia aliposikia sauti hiyo, alijifunika uso kwa koti lake, akatoka na kusimama kwenye mulango wa pango. Halafu, akasikia sauti: “Elia! Unafanya nini hapa?” Naye akasema: “Ninaona uchungu na wivu, ee Yawe, Mungu wa majeshi, kwa sababu watu wa Israeli wamevunja agano lako, wakazibomoa mazabahu zako na kuwaua manabii wako kwa upanga; ni mimi tu niliyebaki, nami vilevile wananiwinda waniue!” Yawe akamwambia: “Urudie kwa kupitia njia ya jangwa mpaka Damasiki. Utakapofika, umupakae Hazaeli mafuta akuwe mufalme wa Aramu. Naye Yehu mwana wa Nimusi, umupakae mafuta akuwe mufalme wa Israeli. Elisha mwana wa Safati wa Abeli-Mehola, utamupakaa mafuta akuwe nabii kwa pahali pako. Basi, mutu yeyote atakayepona kuuawa kwa upanga wa Hazaeli, Yehu atamwua, na yeyote atakayepona kuuawa kwa upanga wa Yehu, Elisha atamwua. Lakini, nitawaacha wazima watu elfu saba katika inchi ya Israeli, ambao hawajainama mbele ya Bali, wala kuibusu sanamu yake.” Elia akaondoka, akamukuta Elisha mwana wa Safati akilima. Pale, kulikuwa makundi kumi na mbili ya ngombe dume wawiliwawili wakilima, na ngombe wawili wa Elisha walikuwa wa nyuma kabisa. Basi, Elia akavua koti lake na kumutupia. Halafu, Elisha akawaacha ngombe wake, akamufuata Elia mbio na kumwambia: “Uniruhusu kwanza niende kumupa baba yangu na mama yangu busu la kwa heri, kisha nikufuate.” Elia akamujibu: “Kwenda! Ni nini niliyokutendea?” Basi, Elisha akamwacha Elia, akarudilia ngombe wake, akawachinja ngombe hao na kuwapika akitumia miti ya nira kama kuni, akawapa watu, wakakula. Kisha akaondoka, akamufuata Elia na kuwa mutumishi wake. Beni-Hadadi mufalme wa Aramu alikusanya waaskari wake wote. Aliungwa mukono na wafalme wengine makumi tatu na wawili pamoja na farasi na magari yao ya vita. Aliuendea muji wa Samaria akauzunguka na kuushambulia. Kisha, akatuma wajumbe wake katika muji kwa mufalme Ahabu wa Israeli, wakamwambia: “Mufalme Beni-Hadadi anasema hivi: ‘Feza na zahabu yako yote ni mali yangu; wake zako wazuri na watoto wako ni wangu vilevile.’ ” Naye mufalme wa Israeli akajibu: “Bwana wangu mufalme, ulivyosema ni sawa: mimi ni wako, na vyote ninavyokuwa navyo ni vyako.” Nyuma, wajumbe wale wakarudia tena kwa Ahabu, wakamwambia: “Mufalme Beni-Hadadi anasema hivi: ‘Nilikutumia ujumbe kwamba unipe zahabu, feza, wake zako pamoja na watoto wako. Sasa, kesho kwa wakati kama huu, nitatuma watumishi wangu wakuje kutafutatafuta ndani ya nyumba yako na nyumba za watumishi wako, watwae na kupeleka kila kitu unachokiona kuwa cha bei kali.’ ” Halafu Ahabu mufalme wa Israeli akawaita viongozi wote wa inchi, akawaambia: “Sasa, muone jinsi mutu huyu anavyotaka kutuletea hasara! Ametuma ujumbe kwamba anataka wake zangu, watoto wangu, zahabu na feza yangu. Nami sikumukatalia!” Wazee na watu wote wakamwambia: “Usimujali wala usikubali.” Basi, Ahabu akawaambia wajumbe wa Beni-Hadadi: “Mumwambie bwana wangu mufalme hivi: ‘Nitafanya yote uliyoomba kwa mara ya kwanza, lakini haya ya pili sikubali hata kidogo.’ ” Hapo, wajumbe hao wakaenda zao na kumupasha tena mufalme Beni-Hadadi. Beni-Hadadi akamutumia Ahabu ujumbe huu: “Miungu iniue ikiwa kule Samaria kutabakia mavumbi ya kutosha kwa kujaza vitanga vya mikono kwa kila mumoja wa watu wangu wengi wanaonifuata!” Mufalme Ahabu wa Israeli akajibu: “Mumwambie mufalme Beni-Hadadi kwamba shujaa anajisifu kisha kupigana vita, na si mbele ya vita!” Beni-Hadadi alipokea ujumbe huu wa Ahabu wakati yeye na wafalme waliomwunga mukono walipokuwa ndani ya mahema yao wakikunywa. Basi, akaweka waaskari wake tayari kwa kuushambulia muji ule. Wakati uleule, nabii mumoja akamwendea Ahabu, mufalme wa Israeli, akamwambia: “Yawe anasema hivi: ‘Unaona wingi wa waaskari hawa? Leo hii nitawatia katika mikono yako, nawe utatambua kwamba mimi ndimi Yawe.’ ” Naye Ahabu akauliza: “Kwa musaada wa nani?” Nabii akasema: “Yawe anasema hivi: ‘Kwa musaada wa vijana wanaotumikia jeshi chini ya maliwali wa majimbo.’ ” Naye mufalme akauliza: “Ni nani atakayeanza kupigana?” Nabii akajibu: “Wewe!” Basi, mufalme Ahabu akachunguza vijana waliotumikia jeshi chini ya maliwali wa majimbo, jumla yao ilikuwa watu mia mbili makumi tatu na wawili. Kisha akachunguza waaskari wa Israeli, walikuwa waaskari elfu saba. Basi, wakati wa saa sita za muchana, Beni-Hadadi na wale wafalme wenzake makumi tatu na wawili waliomwunga mukono walipokuwa katika mahema yao wakikunywa na kulewa, mashambulizi yakaanza. Wale vijana waliotumikia jeshi chini ya maliwali wa majimbo, wakatangulia. Wakati ule, Beni-Hadadi alikuwa amekwisha kupeleka waaskari wapelelezi, nao wakamupa habari kwamba kulikuwa kundi la watu waliokuja kutoka Samaria. Beni-Hadadi akawaambia: “Muwakamate wakiwa wazima. Hata kama wanakuja kwa vita au kwa amani.” Basi, wale vijana waliotumikia jeshi chini ya maliwali wa majimbo, wakaongoza mashambulizi, na huku nyuma yao, waaskari wa Israeli waliwafuata. Kila mumoja wao akamwua adui mumoja. Watu wa Aramu wakakimbia, nao waaskari wa Israeli wakawafuatilia. Lakini Beni-Hadadi mufalme wa Aramu akapanda juu ya farasi, akatoroka na sehemu ya waaskari wapanda-farasi. Basi, mufalme wa Israeli akashinda vita, akateka farasi na magari ya vita mengi, na kuwaua Waaramu kwa wingi. Kisha, yule nabii akamwendea mufalme wa Israeli, akamwambia: “Uongeze nguvu yako, ufikiri vizuri la kufanya. Mwaka kesho, mufalme wa Aramu atakuja kukushambulia tena.” Watumishi wa mufalme Beni-Hadadi walimushauria hivi: “Miungu ya Waisraeli ni miungu ya juu ya milima; ndiyo maana tulishindwa. Lakini, bila shaka tutawashinda kama tukipigana nao katika bonde. Sasa, ufanye hivi: Uwaondoe wale wafalme makumi tatu na wawili katika madaraka yao na kwa pahali pao uweke majemadari. Ukusanye waaskari kama walewale uliopoteza, farasi na magari ya vita kama yale uliyopoteza. Kisha, tutapigana nao katika bonde na bila shaka tutawashinda.” Mufalme Beni-Hadadi akasikia shauri lao, akafanya hivyo. Halafu kwa mwaka uliofuata, mufalme Beni-Hadadi akawakusanya watu wake, akaenda katika muji wa Afeki kwa kupigana na watu wa Israeli. Nao watu wa Israeli walikusanywa na kupewa silaha, wakaenda kupigana na Waaramu. Watu wa Israeli walipiga kambi, wakaonekana kama vikundi vidogovidogo vya mbuzi, lakini Waaramu walijaa katika inchi. Halafu, mutu mumoja wa Mungu akamukaribia mufalme wa Israeli, akamwambia: “Yawe anasema hivi: ‘Kwa sababu Waaramu wamesema kwamba mimi Yawe ni Mungu wa milima wala si Mungu wa inchi ya bonde, nitakupa ushindi juu ya kundi hili kubwa, nawe utatambua kwamba mimi ni Yawe.’ ” Watu wa Israeli na Waaramu walipiga kambi kwa muda wa siku saba, wakielekeana. Siku ya saba, mapigano yakaanza. Siku hiyohiyo, watu wa Israeli wakaua waaskari wa miguu elfu mia moja. Waliobaki, walikimbilia katika muji wa Afeki. Kule, kuta za muji ziliwaangukia na kuwaua watu elfu makumi mbili na saba waliobakia. Beni-Hadadi vilevile alikimbia na kujificha katika chumba fulani cha ndani, katika muji. Watumishi wake wakamwendea, wakamwambia: “Tumesikia kwamba wafalme wa Israeli ni wema. Basi, uturuhusu tujifunge magunia kwenye viuno na kamba katika shingo, tumwendee mufalme wa Israeli. Labda atayaokoa maisha yako.” Basi, wakajifungia magunia kwenye viuno na kamba katika shingo yao, wakamwendea mufalme wa Israeli, wakamwambia: “Mutumishi wako, Beni-Hadadi, anakusihi akisema: ‘Tafazali, uniache nipate kuishi.’ ” Ahabu akasema: “Kumbe angali anaishi? Yeye ni ndugu yangu.” Watumishi wa Beni-Hadadi walitambua kwamba masemi yake yalikuwa kitambulisho kizuri. Kwa hiyo wakasema: “Ndiyo, Ben-hadadi ni ndugu yako!” Ahabu akawaambia: “Mwende mumulete kwangu.” Basi, Beni-Hadadi alipofika, Ahabu akamuruhusu kuikaa pamoja naye katika gari lake la vita. Kisha, Beni-Hadadi akamwambia: “Miji yote ambayo baba yangu alimunyanganya baba yako, nitakurudishia. Unaweza kuanzisha masoko kule Damasiki kama vile baba yangu alivyofanya kule Samaria.” Ahabu akajibu: “Nitakuachilia kwa masharti hayo.” Hapo, akafanya mapatano naye na kumwacha huru. Kwa amri ya Yawe, mumoja wa wanafunzi wa manabii akamwambia mwenzake: “Unipige, tafazali.” Lakini mwenzake akakataa kumupiga. Naye akamwambia: “Kwa sababu umekataa kutii amri ya Yawe, basi, mara tu utakapoachana nami, simba atakuua.” Na kweli, mara tu alipoachana naye, akakutana na simba, akamwua. Kisha, yule mwanafunzi akamukuta mutu mwingine, akamwambia: “Unipige, tafazali.” Mutu yule akamupiga na kumwumiza. Basi, nabii akajifunga kitambaa kwenye uso kusudi asitambuliwe, akaenda, akakaa pembeni ya njia kwa kumungojea mufalme wa Israeli. Mufalme alipokuwa anapita, nabii akamulilia akisema: “Bwana, mimi mutumishi wako nilikuwa kwa mustari wa mbele katika vita. Kukakuja askari mumoja, akaniletea mateka mumoja na kuniambia: ‘Umulinde mutu huyu. Akitoroka utalipa kwa maisha yako wewe peke yako, au kwa bei ya vikoroti elfu tatu vya feza.’ Lakini nilipokuwa nikishugulikashugulika, mutu yule akatoroka.” Mufalme wa Israeli akamwambia: “Ndivyo hukumu yako itakavyokuwa. Umejihukumu mwenyewe.” Hapo, nabii akaondoa harakaharaka kitambaa kwenye uso wake, naye mufalme akamutambua kuwa mumoja wa manabii. Basi, nabii akamwambia mufalme: “Yawe anasema hivi: ‘Umemwachilia akuponyoke mutu ambaye niliamuru auawe. Basi, maisha yake utalipa kwa maisha yako, na watu wake kwa watu wako.’ ” Basi, mufalme wa Israeli akaenda zake kwake Samaria, akijaa chuki na huzuni nyingi. Nyuma ya mambo hayo, Naboti wa muji wa Yezereheli alikuwa na shamba lake la mizabibu kule Yezereheli, karibu na nyumba ya Ahabu, mufalme wa Samaria. Basi, siku moja, Ahabu akamwambia Naboti: “Unipe shamba lako la mizabibu nilifanye shamba la mboga, kwa sababu liko karibu na nyumba yangu. Nitakupa shamba lingine zuri zaidi, au ukitaka nitakulipa feza sawasawa na bei yake.” Lakini, Naboti akamujibu: “Jambo la kukupa wewe urizi nilioupata kwa wazee wangu, Yawe alipitishe mbali.” Hapo, Ahabu akarudi kwake akijaa chuki na huzuni nyingi, kwa sababu Naboti wa Yezereheli alimwambia kwamba hatamupa kile alichorizi kutoka kwa wazee wake. Basi, akalala kwenye kitanda, akaficha uso wake na kukataa chakula. Yezebeli, muke wake, akamwendea na kumwuliza: “Mbona umejaa huzuni ndani ya moyo hata kula haukuli?” Naye akamwambia: “Kwa sababu nilizungumuza na Naboti wa Yezereheli, nikataka aniuzishie shamba lake la mizabibu, au kama akipenda nimupe shamba lingine pahali pa lile. Lakini yeye akaniambia: ‘Sitakupa shamba langu la mizabibu.’ ” Hapo, Yezebeli, muke wake, akamwambia: “Anayetawala Israeli ni nani? Si ni wewe? Amuka, ukule na uchangamuke. Mimi peke yangu nitakupa shamba la mizabibu la Naboti wa Yezereheli.” Basi, Yezebeli akaandika barua kwa jina la Ahabu na kuzipiga muhuri wa mufalme. Kisha akapeleka barua hizo kwa wazee na watu wenye heshima walioishi na Naboti kule katika muji. Barua zenyewe ziliandikwa hivi: “Mutangaze kwa watu kwa kufanya sikukuu ya kufunga kula, mukutane na kumupa Naboti nafasi ya heshima kati ya watu. Kisha, mutafute watenda maovu wawili wapate kumushuhudia na kumushitaki wakisema: ‘Wewe umemutukana Mungu na mufalme.’ Kisha mumupeleke inje, mumwue kwa kumutupia mawe!” Basi, wakaaji wenzake na Naboti, wazee na watu wenye heshima wa muji wa Yezereheli wakafanya kama vile Yezebeli alivyowaagiza. Kwa kufuatana na barua alizowatumia, wakatangaza sikukuu ya kufunga kula, wakakutana na kumuweka Naboti kwenye nafasi ya heshima kati ya watu. Wale watenda maovu wawili wakaikaa kwa kumushuhudia Naboti, kisha wakamushitaki mbele ya watu wote wakisema: “Naboti amemutukana Mungu na mufalme.” Basi, Naboti akapelekwa inje ya muji, akauawa kwa kutupiwa mawe. Kisha, Yezebeli akapelekewa habari kwamba Naboti amekwisha uawa kwa kutupiwa mawe. Mara tu Yezebeli alipopata habari kwamba Naboti amekwisha kufa kwa kutupiwa mawe, akamwambia Ahabu: “Simama! Kwenda utwae lile shamba la mizabibu la Naboti wa Yezereheli ambalo alikataa kukuuzishia. Naboti hayuko muzima tena; amekwisha kufa.” Mara tu Ahabu aliposikia kwamba Naboti amekwisha kufa, akasimama na kwenda kulitwaa shamba la mizabibu la Naboti. Basi, neno la Yawe lilimufikia Elia wa Tisibe kusema hivi: “Simama uende kukutana na Ahabu mufalme wa Israeli, ambaye yuko Samaria. Utamukuta katika shamba la mizabibu la Naboti kwa kulitwaa. Umwambie, Yawe anasema hivi: ‘Umeua na kutwaa mali yake vilevile?’ Umwambie Yawe anasema hivi: ‘Pahali pale imbwa walipoilambulia damu ya Naboti, ndipo watakapoilambulia damu yako.’ ” Basi, Ahabu alipomwona Elia, akasema: “Ewe adui yangu, umeninasa tena?” Elia akamujibu: “Ndiyo! Nimekunasa, kwa sababu wewe umekusudia kabisa kutenda maovu mbele ya Yawe. Basi! Yawe anasema hivi: ‘Hakika, nitakuletea maangamizi. Nitakuletea hasa wewe na kuangamiza kila mwanaume wa ukoo wako katika Israeli, akuwe mutumwa au huru. Jamaa yako nitaifanya kama jamaa ya Yeroboamu mwana wa Nebati, na kama jamaa ya Basha mwana wa Ahiya, kwa sababu umeiwasha hasira yangu na kuwasukuma watu wa Israeli watende zambi.’ Tena, Yawe anasema hivi juu ya Yezebeli: ‘Imbwa wataukula mwili wa Yezebeli humuhumu katika muji wa Yezereheli. Hakika, mutu yeyote wa jamaa yake atakayekufia ndani ya muji, imbwa watamukula; na mutu yeyote atakayekufia katika shamba, ndege watamukula.’ ” Hakuna mutu aliyekusudia kutenda maovu mbele ya Yawe kama Ahabu, ambaye alishawishiwa na Yezebeli, muke wake. Alitenda machukizo kwa kuabudu sanamu za miungu kama vile Waamori walivyofanya ambao zamani Yawe aliwafukuza mbele ya watu wa Israeli. Lakini, Ahabu aliposikia maneno hayo, akapasua nguo zake, akavaa gunia peke yake, akafunga, akakuwa analala na gunia, na kwenda huko na huko kwa huzuni. Basi, neno la Yawe lilimufikia Elia wa Tisibe kusema hivi: “Umeona jinsi Ahabu alivyojinyenyekeza mbele yangu? Basi, kwa sababu amejinyenyekeza, sitaleta yale maangamizi atakapokuwa angali anaishi, lakini nyakati za utawala wa mwana wake nitaiangamiza jamaa ya Ahabu.” Kwa muda wa miaka mitatu hivi, kulikuwa amani kati ya Israeli na Aramu. Lakini katika mwaka wa tatu, Yosafati mufalme wa Yuda alifika kumutembelea Ahabu mufalme wa Israeli. Ahabu akawaambia watumishi wake: “Hamujui kwamba muji wa Ramoti-Gileadi ni mali yetu? Mbona basi tunajiikalia tu bila kuunyanganya kutoka kwa mufalme wa Aramu?” Kisha akamwuliza Yosafati: “Utaandamana nami kwa kupigana kule Ramoti-Gileadi?” Naye Yosafati akamujibu mufalme wa Israeli: “Ndiyo, mimi na wewe ni mutu mumoja, watu wangu ni watu wako, farasi wangu ni farasi wako.” Kisha Yosafati aliendelea kumwambia mufalme wa Israeli: “Lakini, kwanza umwulize Yawe shauri.” Basi, Ahabu akakusanya manabii yapata mia ine, akawauliza: “Niende au nisiende kushambulia Ramoti-Gileadi?” Nao wakamujibu: “Kwenda! Yawe atakupatia ushindi.” Lakini, Yosafati akasema: “Hapa hakuna nabii mwingine wa Yawe ambaye tunaweza kumwomba shauri?” Naye mufalme wa Israeli akamujibu Yosafati: “Kungali mumoja, Mikaya mwana wa Imula. Yeye tunaweza kumwomba shauri la Yawe. Lakini ninamuchukia sana kwa sababu yeye, hatabiri jambo zuri juu yangu hata kidogo, lakini baya tu.” Yosafati akamwambia: “Si vizuri kwa mufalme kusema hivyo.” Basi, Ahabu mufalme wa Israeli akamwita mutumishi mumoja, akamwamuru: “Haraka! Kwenda umulete Mikaya mwana wa Imula.” Wakati ule, mufalme wa Israeli pamoja na Yosafati mufalme wa Yuda walikuwa wakiikaa katika viti vyao vya kifalme, wakiikaa kwenye kiwanja cha kupepetea ngano kwenye mulango wa kuingilia katika muji wa Samaria, nao walikuwa wakivaa nguo zao za kifalme. Wakati ule manabii wote wakakuwa wanatabiri mbele yao. Kisha mumoja wa manabii hao, Zedekia mwana wa Kenana, akajitengenezea pembe za chuma akasema: “Yawe anasema hivi: ‘Kwa pembe hizi, utawarudisha nyuma Waaramu na kuwaangamiza.’ ” Hata wale manabii wengine wote wakatabiri vile vile, wakasema: “Kwenda uushambulie muji wa Ramoti-Gileadi, utashinda! Yawe atautia katika mikono yako.” Wakati ule, yule mutumishi aliyetumwa kwenda kwa Mikaya, akamwambia: “Manabii wengine wote kwa pamoja, wamemutabiria mufalme ushindi. Tafazali, nawe vilevile ufanye kama wao, umutabirie mazuri.” Lakini Mikaya akamujibu: “Kama vile Yawe anavyoishi, mimi nitasema tu yale Yawe atakayoniambia.” Basi, Mikaya alipofika mbele ya mufalme, mufalme akamwuliza: “Twende kupigana vita kule Ramoti-Gileadi au tusiende?” Naye alimujibu: “Kwenda na ufanikiwe, naye Yawe atautia katika mikono yako.” Lakini mufalme akamwambia: “Nitakuapisha mara ngapi kwamba unaposema nami kwa jina la Yawe, unapaswa kuniambia ukweli mutupu?” Halafu, Mikaya akasema: “Niliona watu wote wa Israeli wametawanyika juu ya milima kama kondoo wasiokuwa na muchungaji. Naye Yawe akasema: ‘Watu hawa hawana kiongozi. Basi warudi kila mutu kwake kwa amani.’ ” Hapo, mufalme wa Israeli akamwuliza Yosafati: “Sikukuambia hatatabiri mazuri hata kidogo juu yangu lakini mabaya tu?” Kisha Mikaya akasema: “Sasa sikia neno la Yawe: Nilimwona Yawe akiikaa katika kiti chake cha kifalme, na jeshi lote la mbinguni likisimama pembeni yake, upande wake wa kuume na wa kushoto. Halafu Yawe akauliza: ‘Ni nani atakayemushawishi Ahabu aende aangamie kule Ramoti-Gileadi?’ Kila mumoja akajibu namna alivyofikiri. Kisha pepo mumoja akajitokeza mbele ya Yawe, akasema: ‘Mimi nitamushawishi.’ Yawe akamwuliza: ‘Kwa namna gani?’ Naye akajibu: ‘Nitakwenda na kuwasukuma manabii wake wote waseme uongo.’ Yawe akamwambia: ‘Wewe utamushawishi na utashinda; basi, kwenda ufanye hivyo.’ Basi, ndivyo inavyokuwa: Yawe amewasukuma hawa manabii wako wote waseme uongo. Yawe amesema mabaya juu yako!” Zedekia mwana wa Kenana akamukaribia Mikaya, akamupiga kofi kwenye shavu na kumwuliza: “Tangu wakati gani Roho wa Yawe ameniacha mimi, na kuanza kusema nawe?” Mikaya akamujibu: “Siku utakapoingia katika chumba cha ndani kwa kujificha, ndipo utakapojua.” Naye mufalme wa Israeli akatoa amri: “Mumukamate Mikaya. Mumupeleke kwa Amoni mukubwa wa muji na kwa Yoasi mwana wa mufalme. Uwaambie wamutie katika gereza na kumukulisha mukate kidogo na maji, mpaka nitakaporudi salama.” Halafu Mikaya alisema: “Ukirudi salama basi, utajua kwamba Yawe hakusema nami.” Kisha akaendelea kusema: “Musikilize enyi watu wote!” Basi, mufalme wa Israeli akaenda pamoja na mufalme Yosafati wa Yuda kuushambulia muji wa Ramoti-Gileadi. Mufalme wa Israeli akamwambia Yosafati: “Mimi nitavaa nguo zisizokuwa za kifalme na kuingia katika vita lakini wewe utavaa nguo zako za kifalme.” Hivyo mufalme wa Israeli akaenda kwenye vita bila kuvaa nguo za kifalme. Mufalme wa Aramu alikuwa amewaamuru viongozi wake makumi tatu na wawili waliosimamia magari yake ya vita, akisema: “Musishambulie mutu yeyote, mukubwa au mudogo, lakini tu mufalme wa Israeli.” Nyuma, viongozi hao walipomwona Yosafati, walisema: “Kweli, huyu ndiye mufalme wa Israeli.” Kwa hiyo, walimwelekea, wakamushambulia, lakini Yosafati akapiga kelele. Viongozi walipotambua kwamba hakukuwa mufalme wa Israeli waliacha kumushambulia, wakarudia. Lakini, askari mumoja wa Aramu akauvuta upinde wake kwa kubahatisha, akamupiga mushale mufalme wa Israeli katika maunganio ya nguo zake za chuma za kukinga kifua. Hapo Ahabu akamwambia kiongozi wa gari lake la vita: “Geuza gari uniondoe katika vita. Nimeumizwa!” Na mapigano siku hiyo yakazidi kuwa makali, naye mufalme akiegemeshwa ndani ya gari, akiwaelekea Waaramu. Ilipofika magaribi, akakufa. Damu ikakuwa inamutoka kwenye kidonda chake na kutiririka mpaka chini ya gari. Jua liliposhuka, amri ikatolewa: “Kila mutu arudie kwake! Kila mutu arudie kwake!” Mufalme Ahabu alikufa na maiti yake ilipelekwa Samaria, ikazikwa kule. Gari lake la vita walilisafisha katika kisima cha Samaria, imbwa wakailamba damu yake, nao makahaba wakaoga mule, sawa kabisa na neno Yawe alilosema. Mambo mengine ya Ahabu, yote aliyofanya, na jinsi alivyojenga na kupamba nyumba yake kwa pembe, na miji yote aliyojenga, yote yameandikwa katika Kitabu cha Mambo ya Siku za Wafalme wa Israeli. Ahabu alipokufa, mwana wake Ahazia alitawala kwa pahali pake. Katika mwaka wa ine wa utawala wa mufalme Ahabu wa Israeli, Yosafati mwana wa Asa alianza kutawala Yuda. Yosafati alikuwa na umri wa miaka makumi tatu na mitano alipoanza kutawala. Alitawala akiwa Yerusalema kwa muda wa miaka makumi mbili na mitano. Mama yake aliitwa Azuba binti ya Silihi. Alitenda mema mbele ya Yawe kama vile baba yake Asa alivyofanya. Lakini hakuharibu nafasi ya kutambikia juu ya vilima. Watu waliendelea kutambikia na kufukiza ubani kwa nafasi ile. Yosafati vilevile, alifanya mapatano ya amani na mufalme wa Israeli. Matendo mengine ya Yosafati, ushujaa wake na vita alivyopigana, yote yameandikwa katika Kitabu cha Mambo ya Siku za Wafalme wa Yuda. Waasherati wote wa kidini waliobaki tangu nyakati za baba yake Asa, Yosafati aliwaondoa katika inchi. Katika inchi ya Edomu, hakukuwa mufalme. Inchi hiyo ilitawaliwa na musimamizi. Mufalme Yosafati alitengeneza mashua za kwenda Ofiri kuleta zahabu, lakini hazikufika kwa sababu zilivunjikavunjika kule Esioni-Geberi. Basi, Ahazia mwana wa Ahabu akamwambia Yosafati: “Uwaache watumishi wangu wasafiri pamoja na watumishi wako katika mashua.” Lakini Yosafati hakukubali jambo hilo. Kwa mwisho, Yosafati akakufa, akazikwa pamoja na babu zake katika makaburi ya kifalme katika muji wa Daudi babu yake. Naye Yoramu mwana wake akatawala kwa pahali pake. Katika mwaka wa kumi na saba wa utawala wa Yosafati mufalme wa Yuda, Ahazia mwana wa Ahabu alianza kutawala Israeli. Alitawala kwa muda wa miaka miwili, akiwa Samaria. Ahazia alitenda maovu mbele ya Yawe; alifuata mwenendo wa baba yake na mwenendo wa mama yake Yezebeli, na wa Yeroboamu mwana wa Nebati ambaye aliwasukuma watu wa Israeli watende zambi. Alimutumikia na kumwabudu Bali, akamukasirikisha Yawe, Mungu wa Israeli, kwa kila jambo kama vile baba yake alivyofanya. Kisha kufa kwa Ahabu, watu wa Moabu waliasi wasitawaliwe na Israeli. Mufalme Ahazia alipokuwa Samaria alianguka kutoka chumba kilichokuwa juu ya paa ya nyumba yake, akaumia vibaya. Kwa hiyo akawatuma wajumbe, akawaambia: “Muende kwa Bali-Zebubu, mungu wa muji wa Ekuroni, mumwulize kama nitapona ugonjwa huu.” Lakini malaika wa Yawe akamwambia nabii Elia wa muji wa Tisibe, aende kukutana na wajumbe hao na kuwauliza: “Kwa nini munakwenda kwa Bali-Zebubu, mungu wa Ekuroni? Hakuna Mungu katika inchi ya Israeli? Mumwambie mufalme kwamba Yawe amesema hivi: ‘Hautashuka katika kitanda ulichopanda juu yake. Hakika utakufa.’ ” Basi, Elia akawaendea. Wale wajumbe wakarudi kwa mufalme, naye akawauliza: “Mbona mumerudia?” Wakamujibu: “Tumekutana na mutu ambaye alitutuma turudi kukuambia kwamba Yawe amesema hivi: ‘Kwa nini unatuma wajumbe kwa Bali-Zebubu, mungu wa Ekuroni? Hakuna Mungu katika inchi ya Israeli? Hautashuka katika kitanda ulichopanda juu yake. Hakika utakufa.’ ” Mufalme akauliza: “Ni mutu gani yule aliyekutana nanyi na kuwaambia mambo hayo?” Wao wakamujibu: “Alikuwa akivaa nguo ya manyoya na mukaba wa ngozi kwenye kiuno.” Mufalme akasema: “Yule ni Elia wa Tisibe!” Halafu akamutuma kiongozi mumoja wa waaskari na watu wake makumi tano wamulete Elia. Kiongozi huyo akaenda, akamukuta Elia akiikaa kwenye mulima, akamwambia: “Ewe mutu wa Mungu, mufalme anakuamuru ushuke.” Elia akamujibu yule kiongozi wa watu makumi tano: “Kama kweli mimi ni mutu wa Mungu, moto ushuke kutoka mbinguni na kukuteketeza wewe pamoja na watu wako!” Mara moja moto ukashuka kutoka mbinguni, ukamuteketeza pamoja na watu wake makumi tano. Mufalme akamutuma kiongozi mwingine na watu wake makumi tano wamulete Elia. Naye akamwambia Elia: “Ewe mutu wa Mungu, mufalme anakuamuru ushuke mara moja!” Elia akamujibu: “Kama kweli mimi ni mutu wa Mungu, moto ushuke kutoka mbinguni na kukuteketeza wewe pamoja na watu wako!” Mara moja moto wa Mungu ukashuka kutoka mbinguni, ukamuteketeza pamoja na watu wake makumi tano. Kwa mara ingine tena, mufalme akatuma kiongozi mwingine na watu wake makumi tano. Kiongozi wa tatu akapanda kwenye mulima, akapiga magoti mbele ya Elia na kumusihi akisema: “Ewe mutu wa Mungu, ninakusihi uyahesabu maisha yangu na maisha ya hawa watumishi wako makumi tano yakuwe ya bei kali mbele yako. Viongozi wawili waliotangulia na watu wao, wameteketezwa na moto ulioshuka toka mbinguni; lakini sasa ninakuomba uhurumie maisha yangu.” Malaika wa Yawe akamwambia Elia: “Shuka pamoja naye, wala usimwogope.” Basi, Elia akasimama, akashuka pamoja naye mpaka kwa mufalme. Akamwambia mufalme: “Yawe anasema hivi: ‘Kwa sababu ulituma wajumbe kuomba shauri kwa Bali-Zabubu mungu wa Ekuroni sawa vile hakuna Mungu katika Israeli ambaye ungemwomba shauri, basi, hautashuka katika kitanda ambacho umepanda juu yake. Hakika utakufa.’ ” Kisha Ahazia akakufa kama vile Yawe alivyomwambia nabii wake Elia. Na kwa sababu Ahazia hakukuwa na mutoto mwanaume, Yoramu akakuwa mufalme kwa pahali pake, katika mwaka wa pili wa utawala wa Yehoramu mwana wa Yosafati, mufalme wa Yuda. Mambo mengine mufalme Ahazi aliyoyatenda yameandikwa katika Kitabu cha Mambo ya Siku za Wafalme wa Israeli. Wakati ulifika ambapo Yawe alitaka kumupandisha Elia mbinguni katika upepo wa kuzungukazunguka. Elia na Elisha walikuwa katika njia, wakitoka Gilgali. Walipokuwa katika njia, Elia akamwambia Elisha: “Tafazali ubakie hapa. Yawe amenituma niende Beteli.” Lakini Elisha akamwambia: “Kama vile Yawe anavyoishi na kama vile unavyoishi, sitakuacha.” Basi, wakaenda pamoja mpaka Beteli. Wanafunzi wa manabii wa Beteli wakamwendea Elisha, wakamwuliza: “Unajua kwamba leo Yawe atamupeleka bwana wako?” Elisha akajibu: “Ndiyo. Ninajua. Munyamaze.” Kisha Elia akamwambia Elisha: “Tafazali ubakie hapa. Yawe amenituma niende Yeriko.” Lakini Elisha akakataa akisema: “Kama vile Yawe anavyoishi na kama vile unavyoishi, sitakuacha.” Basi, wakaenda pamoja mpaka Yeriko. Wanafunzi wa manabii wa Yeriko wakamwendea Elisha, wakamwuliza: “Unajua kwamba leo Yawe atamupeleka bwana wako?” Elisha akawajibu: “Ndiyo. Ninajua. Munyamaze.” Kisha Elia akamwambia Elisha: “Tafazali ubakie hapa. Yawe amenituma niende Yordani.” Lakini Elisha akasema: “Kama vile Yawe anavyoishi na kama vile unavyoishi, sitakuacha.” Basi, wakaenda pamoja. Manabii makumi tano wakawafuata mpaka kwenye muto Yordani. Elia na Elisha wakasimama karibu na muto, nao manabii wakasimama mbali kidogo. Elia akavua nguo yake, akaikunja na kupiga nayo maji. Maji yakagawanyika katika sehemu mbili, nao wakavuka mpaka ngambo, wakipitia pahali pakavu. Walipofika ngambo, Elia akamwambia Elisha: “Uniambie jambo unalotaka nikufanyie mbele sijaondolewa kwako.” Elisha akamwambia: “Ninaomba sehemu mara mbili ya roho yako.” Elia akajibu: “Ombi lako ni gumu. Hata hivyo, ikiwa utaniona wakati nitakapoondolewa kwako, itafanyika vile kwako. Lakini usiponiona, basi haitafanyika vile.” Walipokuwa wanatembea na kuongea, kwa rafla gari la moto lililokokotwa na farasi wa moto likawatenganisha. Naye Elia akanyanyuliwa mbinguni katika upepo wa kuzungukazunguka. Elisha alipoona tukio hilo, akalia: “Baba yangu, baba yangu! Ulikuwa wa lazima kuliko magari ya Israeli na wapanda-farasi wake!” Basi, Elisha hakumwona tena Elia. Halafu Elisha akashika nguo zake na kuzipasua vipande viwili. Kisha akaokota nguo ya Elia iliyomwangukia, akarudia na kusimama kwenye ukingo wa muto Yordani. Akayapiga maji kwa nguo ya Elia akisema: “Yuko wapi Yawe, Mungu wa Elia?” Alipopiga maji, yakagawanyika sehemu mbili, naye akavuka mpaka ngambo. Wale wanafunzi wa manabii kutoka Yeriko walipomwona, walisema: “Roho wa Elia yuko kwa Elisha.” Basi, wakaenda kumupokea, wakainama mbele yake kwa heshima. Wakamwambia: “Sisi watumishi wako tuko na mashujaa makumi tano. Tafazali, uwaruhusu waende kumutafuta bwana wako. Labda roho wa Yawe amemubeba na kumutupa juu ya mulima fulani au katika bonde.” Elisha akajibu: “Hapana, musiwatume.” Lakini wao walimwuzi sana mpaka akaona haya, akawaambia: “Muwatume.” Hivyo wakawatuma watu makumi tano, wakaenda wakamutafuta kila fasi kwa muda wa siku tatu nao hawakumwona. Kisha wakarudi kwa Elisha aliyekuwa anawangojea kule Yeriko. Elisha akawauliza: “Sikuwaambia musiende?” Kisha watu wa Yeriko wakamwendea Elisha, wakamwambia: “Bwana, kama vile unavyoona, muji huu ni muzuri, lakini maji tunayokuwa nayo ni mabaya na yanasababisha mimba kuharibika.” Elisha akawaambia: “Mutie chumvi ndani ya bakuli jipya, kisha muniletee.” Nao wakamuletea. Elisha akaenda kwenye chemichemi ya maji, akatupa chumvi hiyo ndani na kusema: “Yawe anasema hivi: Nimeyafanya maji haya kuwa yenye kufaa. Tangu sasa hayatasababisha vifo au kutoa mimba.” Na maji hayo yakakuwa ya kufaa mpaka leo, kama vile Elisha alivyosema. Elisha aliondoka Yeriko, akaenda Beteli. Alipokuwa katika njia, vijana wamoja walitoka katika muji, wakaanza kumuzomea wakisema: “Kwenda zako, kwenda zako muzee wa upaa!” Elisha aligeuka, akawaangalia na kuwalaani kwa jina la Yawe. Dubu wawili wakatoka katika pori, wakawararua vijana makumi ine na wawili kati yao. Elisha akaendelea na safari yake mpaka kwenye mulima Karmeli na tokea kule akarudi Samaria. Katika mwaka wa kumi na nane wa utawala wa mufalme Yosafati wa Yuda, Yoramu mwana wa Ahabu alianza kutawala inchi ya Israeli. Akatawala akiwa Samaria kwa muda wa miaka kumi na miwili. Yoramu alitenda maovu mbele ya Yawe, lakini yeye hakukuwa mubaya kama baba na mama yake; maana alibomoa munara wa Bali uliofanywa na baba yake. Hata hivyo, Yoramu aliendelea kutenda zambi ileile ya Yeroboamu mwana wa Nebati ambaye aliwasukuma watu wa Israeli watende zambi. Hakuiacha. Mufalme Mesha wa Moabu alikuwa mufugaji wa kondoo, na kila mwaka alilipa kodi kwa mufalme wa Israeli wana-kondoo elfu mia moja na manyoya ya kondoo wengine elfu mia moja. Lakini Ahabu alipokufa, mufalme wa Moabu alimwasi. Kwa hiyo mufalme Yoramu akaondoka Samaria, akakusanya waaskari wote wa Israeli. Akatuma ujumbe kwa mufalme Yosafati wa Yuda, akamwambia: “Mufalme wa Moabu ameniasi. Utashirikiana nami tupigane naye?” Mufalme Yosafati akamujibu: “Niko tayari! Mimi na wewe ni kitu kimoja; watu wangu ni kama wako, farasi wangu ni kama wako. Tutashambulia kutokea upande gani?” Yoramu akajibu: “Tutashambulia kutokea jangwa la Edomu.” Basi, mufalme Yoramu akaondoka pamoja na mufalme wa Yuda na mufalme wa Edomu. Nyuma ya kusafiri kwa muda wa siku saba, maji yakawaishia. Hawakukuwa na maji kwa ajili ya waaskari wao wala kwa nyama wao. Hapo mufalme wa Israeli akasema: “Ole wetu! Yawe ametukusanya wote wafalme watatu atutie katika mikono ya mufalme wa Moabu.” Mufalme Yosafati akauliza: “Hakuna nabii yeyote hapa wa Yawe ambaye tunaweza kumwuliza shauri la Yawe?” Mutumishi mumoja wa mufalme Yoramu wa Israeli akajibu: “Elisha mwana wa Safati iko hapa. Yeye alikuwa mutumishi wa Elia.” Yosafati akasema: “Huyo ni nabii wa kweli.” Kisha wafalme hao watatu wakamwendea Elisha. Elisha akamwuliza mufalme wa Israeli: “Kuna maneno gani kati yako nami? Kwenda uombe shauri kwa manabii ambao baba yako na mama yako waliwaendea.” Mufalme wa Israeli akajibu: “Sivyo! Yawe ndiye aliyetuita sisi wafalme watatu kusudi atutie katika mikono ya mufalme wa Moabu.” Elisha akasema: “Kama vile Yawe wa majeshi, yule ambaye mimi ninamutumikia, anavyoishi, kama isingekuwa kwa heshima ninayokuwa nayo kwa rafiki yako mufalme Yosafati wa Yuda, nisingekujali hata kidogo. Lakini sasa uniletee mupiga kinanda.” Wakamuletea mupiga kinanda. Ikakuwa wakati alipopiga kinanda, nguvu ya Yawe ikamujaza Elisha, akasema: “Yawe anasema hivi: ‘Muchimbe mashimo kila pahali katika bonde.’ Ingawa hamutaona upepo wala mvua, bonde litajaa maji, nanyi mutakunywa, ninyi pamoja na ngombe wenu na nyama wenu. Lakini hili si jambo gumu kwa Yawe; yeye atawapa vilevile ushindi juu ya Moabu. Mutashinda kila muji wenye kuta na kila muji muzuri; mutaikata miti yao yote, mutaziba chemichemi zote za maji, na kuyaharibu mashamba yao yote yenye mboleo kwa kuyajaza mawe.” Kesho yake asubui, wakati wa kutoa sadaka, maji yakatiririka kutoka upande wa Edomu na kujaa kila pahali katika bonde. Wamoabu walipopata habari kwamba hao wafalme watatu wamekuja kuwashambulia, watu wote walioweza kubeba silaha kuanzia vijana mpaka wazee, waliitwa, wakapewa silaha na kuwekwa kwenye mupaka tayari kwa vita. Walipoamuka asubui iliyofuata, jua lilikuwa linametameta juu ya maji hayo; walipoyaangalia yakaonekana kuwa mekundu kama damu. Wakasema: “Hii ni damu! Bila shaka hawa wafalme watatu wamepigana wao kwa wao na kuuana! Tuende tunyanganye vitu vyao!” Lakini walipofika katika kambi ya Waisraeli, watu wa Israeli waliwashambulia, nao wakakimbia mbele yao. Watu wa Israeli wakawafuatilia mpaka Moabu, wakiwaua na kuibomoa miji yao. Kila nafasi walipopita kwenye shamba zuri, kila mutu alilirushia jiwe mpaka kila shamba likajaa mawe; vilevile wakaziziba chemichemi zote za maji na kukata miti yote mizuri. Nyuma ya hayo, kukabaki muji mukubwa wa Kiri-Haraseti peke yake, ambao waaskari wapiga-kombeo waliuzunguka na kuuteka. Mufalme wa Moabu alipoona kwamba vita inamwendea vibaya, akatwaa watu wake mia saba wenye kupigana kwa mapanga, akikusudia kupenya kati ya waaskari wa waadui zake mbele ya mufalme wa Edomu, lakini hakuweza. Hapo akamutwaa mwana wake wa kwanza ambaye angekuwa mufalme kwa pahali pake, akamutoa kuwa sadaka ya kuteketezwa juu ya ukuta wa muji. Watu wa Israeli walipoona hayo, wakachukizwa sana. Wakauacha muji ule na kurudia katika inchi yao. Basi, mwanamuke mumoja kati ya wake za wanafunzi wa manabii akamwendea Elisha, akamwambia: “Mutumishi wako, mume wangu amekufa, na kama vile unavyojua, alikuwa mwenye kumwogopa Mungu. Lakini mutu aliyemukopesha feza amekuja kuwatwaa wana wangu wawili wakuwe watumwa wake.” Elisha akamwuliza: “Sasa nikusaidie namna gani? Uniambie kile unachokuwa nacho kwako.” Mama yule mujane akamujibu: “Mimi mutumishi wako sina kitu chochote lakini chupa ndogo ya mafuta.” Elisha akamwambia: “Kwenda kwa jirani zako, uazime vyombo vitupu vingi vya kutosha. Kisha uende, wewe pamoja na wana wako, mujifungie ndani ya nyumba, na muanze kujaza mafuta. Kila chombo munachojaza, mukiweke pembeni.” Akaenda na kujifungia ndani ya nyumba na wana wake na kuanza kumimia mafuta ndani ya vyombo. Vilipojaa vyote, akamwambia mwana wake mumoja: “Uniletee chombo kingine.” Mwana wake akamujibu: “Vyote vimejaa!” Hapo mafuta yakakoma kutiririka. Akarudi kwa mutu wa Mungu na kumweleza habari hiyo. Naye mutu wa Mungu akamwambia: “Kwenda uuzishe hayo mafuta na kulipa madeni yako, ndipo wewe na wana wako mutaishi kwa kutumia hayo yatakayobaki.” Siku moja Elisha alikwenda Sunemu, ambako kulikuwa mama mumoja tajiri. Mama yule akamwalika Elisha kwa chakula, na toka siku hiyo ikakuwa kawaida Elisha kula chakula kwake kila mara alipopitia kule. Mama yule akamwambia mume wake: “Sina shaka kwamba mutu huyu anayefika kwetu kila mara ni mutakatifu wa Mungu. Ninakuomba basi tumujengee chumba na kule tumwekee kitanda, meza, kiti na taa, kusudi akitumie kila mara anapotutembelea.” Siku moja Elisha akafika kule na kuingia ndani ya chumba chake kusudi apumzike. Akamwambia mutumishi wake Gehazi: “Umwite yule mama Musunami.” Alipomwita akakuja na kusimama mbele yake. Naye Elisha akamwambia Gehazi: “Umwambie, tumeona jinsi alivyotushugulikia; sasa anataka tumutendee jambo gani? Angependa aombewe lolote kwa mufalme au kwa jemadari wa waaskari?” Mama Musunami akamujibu: “Mimi ninaishi kati ya watu wangu.” Elisha akasema: “Tumufanyie nini basi?” Gehazi akamujibu: “Hakika hana mutoto, na mume wake amekuwa muzee.” Elisha akamwambia: “Umwite.” Naye akamwita. Akakuja na kusimama kwenye mulango. Elisha akamwambia: “Mwaka kesho, kwa wakati kama huu, utakuwa na mutoto katika mikono yako.” Mama akamujibu: “Hapana, Bwana wangu! Wewe ni mutu wa Mungu; usinidanganye mimi mutumishi wako!” Lakini yule mwanamuke akapata mimba na kuzaa mutoto wakati kama ule mwaka uliofuata, kama vile Elisha alivyokuwa amemwambia. Mutoto yule alipokomaa, alitoka siku moja pamoja na baba yake akafuatana na wavunaji, naye akamwambia baba yake: “Ole, kichwa changu! Ninaumwa na kichwa!” Baba yake akamwambia mutumishi wake mumoja: “Umupeleke kwa mama yake.” Alipofikishwa kwa mama yake, aliikaa juu ya magoti ya mama yake mpaka saa sita za muchana, halafu akakufa. Mama yake akamupeleka na kumulalisha kwenye kitanda cha mutu wa Mungu, akaufunga mulango na kuondoka. Akamwita mume wake na kumwambia: “Unipe mutumishi mumoja na punda mumoja, kusudi nimwendee mara moja yule mutu wa Mungu, kisha nitarudi.” Mume wake akamwuliza: “Kwa nini unataka kumwona leo? Leo si sikukuu ya mwandamo wa mwezi wala Sabato.” Akamujibu: “Si neno.” Akatandika punda na kumwambia mutumishi: “Sasa kaza mwendo, wala usipunguze mpaka nitakapokuambia.” Basi, akaondoka, akaenda mpaka kwenye mulima Karmeli kule mutu wa Mungu alipokuwa. Mutu wa Mungu alipomwona akikuja, akamwambia Gehazi mutumishi wake: “Angalia, ninamwona Musunami akikuja. Kimbia mara moja kumupokea na kumwuliza: ‘Uko muzima? Mume wako ni muzima? Mutoto ni muzima?’ ” Naye Musunami akamujibu: “Tuko wazima.” Alipofika kwenye mulima kwa mutu wa Mungu, akamushika miguu, naye Gehazi akakaribia kusudi amwondoe. Lakini mutu wa Mungu akamwambia: “Umwache, maana ana uchungu mukali, naye Yawe hakunijulisha jambo hilo.” Huyo mama akamwambia: “Bwana wangu, mimi nilikuomba mutoto? Sikukusihi kwamba usinipatie matumaini ya uongo?” Elisha akamwambia Gehazi: “Ujitayarishe kusafiri, twaa fimbo yangu, na uende mara moja. Usisimame katika njia kwa kumusalimia mutu yeyote, na mutu yeyote akikusalimia katika njia, usipoteze wakati kwa kumurudishia salamu. Kwenda moja kwa moja mpaka katika nyumba na kuweka fimbo yangu juu ya uso wa mutoto.” Mwanamuke akamwambia Elisha: “Kama vile Yawe anavyoishi na kama vile unavyoishi, sitakuacha.” Basi Elisha akaondoka na kufuatana naye. Gehazi akatangulia mbele, na alipofika akaweka fimbo ya Elisha juu ya uso wa mutoto, lakini hakukuonekana kitambulisho chochote cha uzima. Akarudi na kukutana na Elisha, akamwambia: “Kijana hakuamuka.” Elisha alipofika, akaingia peke yake ndani ya chumba na kuona maiti ya kijana kwenye kitanda. Basi, akafunga mulango na kumwomba Yawe. Halafu akajilaza juu ya mutoto, kinywa chake juu ya kinywa cha mutoto, na macho yake juu ya macho ya mutoto na mikono yake juu ya mikono ya mutoto. Na alipokuwa amekaa hivyo, mwili wa mutoto ukaanza kupata joto. Elisha akasimama na kutembeatembea ndani ya chumba, kisha akarudi na kujilaza tena juu ya mutoto. Mutoto akapiga chafya mara saba, halafu akafungua macho. Elisha akamwita Gehazi na kumwambia: “Umwite yule Musunami.” Alipoitwa Elisha akamwambia: “Kamata mwana wako.” Akainama kwenye miguu ya Elisha kwa shukrani na kumukamata mwana wake. Elisha akarudi Gilgali wakati katika inchi kulikuwa njaa. Siku moja, alipokuwa akifundisha wanafunzi wa manabii alimwambia mutumishi wake: “Weka chungu kikubwa juu ya moto, uwapikie manabii chakula.” Mumoja wao akaenda katika shamba na kuchuma mboga. Kule akaona mboga za pori, akachuma mboga nyingi kwa kadiri alivyoweza kubeba. Akakuja nazo, akazikatakata na kuzitia ndani ya chungu bila kuzijua. Chakula kikapakuliwa. Lakini walipokionja wakamulilia Elisha wakisema: “Ee mutu wa Mungu, chakula hiki kitatuua!” Nao hawakuweza kukikula. Elisha akaagiza aletewe unga. Akaletewa unga, naye akautia ndani ya chungu na kusema: “Sasa uwape chakula wakule.” Wakakikula, na hapo hakikuwazuru. Mutu mumoja akatoka Bali-Salisa, akamuletea Elisha mikate makumi mbili iliyotengenezwa kwa shayiri ya malimbuko ya mavuno ya mwaka ule na masuke mabichi ya ngano katika gunia. Elisha akamwagiza Gehazi awape watu wakule. Mutumishi wake akasema: “Sitawapa kwa sababu hakitawatosha watu mia moja”. Elisha akasema: “Uwape wakule, kwa sababu Yawe amesema kwamba watakula na kushiba na kingine kitabaki.” Mutumishi wake akawatayarishia chakula, wakakula na kushiba, na kingine kikabaki, kama vile Yawe alivyosema. Namani, jemadari wa waaskari wa mufalme wa Aramu, alikuwa mutu mukubwa aliyeheshimiwa sana na bwana wake, maana kwa njia yake Yawe aliiletea inchi ya Waaramu ushindi. Alikuwa askari hodari, lakini alikuwa na ugonjwa wa ukoma. Katika vita walivyokuwa wakipigana na Waisraeli, Waaramu walikuwa wamemukamata binti mumoja mudogo kutoka Israeli kuwa mufungwa, naye akakuwa anamutumikia muke wa Namani. Siku moja akamwambia bibi yake, muke wa Namani: “Ingekuwa heri bwana wangu angekwenda na kumwona yule nabii anayekuwa Samaria! Angemuponyesha ugonjwa wake.” Namani alipopata habari hii, akaenda kwa mufalme na kumwelezea habari za mutoto yule. Mufalme wa Aramu akamwambia: “Twaa barua hii umupelekee mufalme wa Israeli.” Hivyo Namani akaondoka, akipeleka vikoroti elfu makumi tatu vya feza, vikoroti elfu sita vya zahabu na nguo kumi za sikukuu. Barua yenyewe iliandikwa hivi: “Ninakutumia jemadari wangu Namani pamoja na barua hii, kusudi upate kumuponyesha ugonjwa wake.” Mufalme wa Israeli aliposoma barua hii alipasua nguo yake na kusema: “Sababu gani mufalme wa Aramu anataka nimuponyeshe mutu huyu ukoma wake? Anafikiri kwamba mimi ni Mungu anayekuwa na uwezo wa kuua au kufufua? Mufahamu basi, muone kwamba mutu huyu anataka kuniletea ugomvi!” Elisha, nabii wa Mungu, alipopata habari kwamba mufalme wa Israeli amepasua nguo zake, alituma ujumbe kwa mufalme, akamwuliza: “Kwa sababu gani umepasua nguo zako? Umutume mutu huyo kwangu, kusudi apate kujua kwamba kuna nabii katika Israeli!” Namani akaenda na farasi wake na gari lake mpaka kwenye mulango wa Elisha. Elisha akamutuma mutumishi wake amwambie: “Kwenda uoge mara saba katika muto Yordani, nawe utapona kabisa.” Lakini Namani alikasirika sana, akaenda zake akisema: “Nilizani kwamba hakika atanifikia na kumwomba Yawe, Mungu wake, apitishe mikono yake juu ya pahali ninapogonjwa na kuniponyesha! Zaidi ya ile, mito Abana na Farpari ya kule Damasiki si bora kuliko mito yote ya Israeli? Nisingeweza kuoga mule na kupona?” Akaondoka na kurudi kwake, naye alikasirika sana. Watumishi wake wakamwendea na kumwambia: “Baba yetu, kama nabii angekuambia ufanye jambo fulani gumu, haungelifanya? Sasa, aliyokuambia tu ni: ‘Ujioshe, kusudi upone!’ ” Basi, Namani akateremuka kwenye muto Yordani akajitumbukiza mule mara saba, kama alivyoagizwa na Elisha mutu wa Mungu, naye akapona kabisa. Ngozi yake ikakuwa laini na yenye afya kama ya mutoto mudogo. Halafu akarudi kwa mutu wa Mungu pamoja na watu wake, akasema: “Sasa ninajua kwamba hakuna Mungu yeyote katika dunia lakini tu Mungu wa Israeli; kwa hiyo, tafazali sasa upokee zawadi ya mutumishi wako.” Elisha akamujibu: “Kama vile Yawe, yule ambaye mimi ninamutumikia, anavyoishi, sitapokea zawadi yoyote.” Namani akamusihi, lakini Elisha akakataa kabisa. Namani akasema: “Ikiwa hautapokea zawadi zangu, basi tafazali umupatie mutumishi wako udongo unaoweza kubebwa na nyumbu wawili, maana tokea leo mimi mutumishi wako sitatoa sadaka za kuteketezwa wala sadaka kwa miungu mingine lakini tu kwa Yawe. Naye Yawe anisamehe ninapofuatana na mufalme wangu kwenda kuabudu katika hekalu la Rimoni mungu wa Waaramu. Ninapaswa kuinama pamoja naye kwa sababu anaegemea kwenye mukono wangu. Ninaomba Yawe anisamehe!” Elisha akamwambia: “Kwenda kwa amani.” Namani akaenda zake. Alipokuwa bado hajafika mbali, Gehazi, mutumishi wa Elisha mutu wa Mungu, akasema: “Bwana wangu amemwachilia Namani wa Aramu aende bila kupokea chochote alicholeta. Kama vile Yawe anavyoishi, nitamufuata kusudi nipate kitu kutoka kwake.” Hapo akaondoka na kumufuata Namani. Namani alipoangalia na kuona mutu anamufuata mbio, akashuka ndani ya gari lake, akaenda kukutana naye. Basi, akamwuliza: “Kuna usalama?” Gehazi akajibu: “Mambo yote ni sawa lakini tu bwana wangu amenituma nikuambie kwamba sasa hivi amepokea watu wawili wa kundi la manabii katika inchi ya milima ya Efuraimu, naye angependa uwape vikoroti elfu tatu vya feza na nguo mbili ya sikukuu.” Namani akasema: “Tafazali twaa vikoroti elfu sita vya feza.” Akamusihi, kisha akamufungia mafungu mawili na kumupa nguo mbili ya sikukuu, akawapa watumishi wake wawili na kuwaagiza wafuatane na Gehazi. Walipofika juu ya mulima pahali Elisha alipoishi, Gehazi akatwaa mafungu ya feza kutoka kwa watumishi wa Namani na kuyapeleka ndani ya nyumba yake. Kisha akawaruhusu wale watumishi waende zao, nao wakaondoka. Halafu Gehazi akaingia kwa Elisha na kuanza kumutumikia. Elisha akamwuliza: “Unatoka wapi?” Gehazi akajibu: “Sikuenda nafasi yoyote.” Lakini Elisha akamwambia: “Unafikiri roho yangu haikukuwa pamoja nawe wakati mutu yule alipotoka ndani ya gari lake na kuja kukutana nawe? Huu ndio wakati wa kupokea feza na nguo, mashamba ya mizeituni na mizabibu, kondoo na ngombe au watumishi na wajakazi? Kwa hiyo ukoma wa Namani utakushika wewe, na wazao wako milele.” Basi, Gehazi aliondoka akiwa ameshikwa na ukoma, na ngozi yake ilikuwa nyeupe kama teluji. Siku moja, wanafunzi wa manabii walimulalamikia Elisha wakisema: “Pahali hapa tunapokaa ni padogo sana kwetu! Uturuhusu tuende Yordani tukate kila mutu muti mumoja kusudi tujijengee pahali pa kututoshelea.” Elisha akawajibu: “Mwende.” Mumoja wao akamwomba akisema: “Tafazali ninakusihi uende pamoja na watumishi wako.” Naye akajibu: “Nitakwenda.” Hivyo akaenda pamoja nao, na walipofika kwenye muto Yordani wakaanza kukata miti. Mumoja wao alipokuwa anakata miti, shoka lake likachomoka na kuanguka ndani ya maji. Akalia, akisema: “Sasa bwana wangu nitafanya nini? Shoka hili tulikuwa tumeliazima!” Elisha akauliza: “Liliangukia wapi?” Mutu huyo akamwonyesha. Elisha akakata kijiti na kukitupa ndani ya maji na palepale shoka likaelea juu ya maji. Elisha akamwamuru alikamate naye akanyoosha mukono, akalikamata. Wakati mumoja kulikuwa vita kati ya Aramu na Israeli. Basi, mufalme wa Aramu akafanya shauri na wakubwa wa waaskari wake juu ya pahali watakapopiga kambi. Lakini Elisha akamupelekea mufalme wa Israeli habari afanye angalisho na pahali pale, kwa sababu Waaramu walikuwa tayari kupashambulia. Basi, mufalme wa Israeli akapeleka waaskari wake karibu na pahali alipoambiwa. Elisha aliendelea kumwonya mufalme naye mufalme alijiweka katika hali ya angalisho. Jambo hilo lilifanyika mara nyingi. Mufalme wa Aramu akafazaishwa sana na hali hiyo. Akawaita wakubwa wa waaskari wake, akawauliza: “Muniambie ni nani kati yenu anayekuwa upande wa mufalme wa Israeli?” Mumoja wao akajibu: “Hakuna anayekuwa upande wake, ee mufalme. Anayefanya vile ni Elisha, nabii anayekuwa kule Israeli. Yeye anamwambia mufalme wa Israeli mambo yote unayosema hata ukiwa katika chumba chako cha kulala.” Mufalme akawaambia: “Mwende mupeleleze mujue pahali anapokuwa nami nitawatuma watu wamukamate.” Basi, wakamwambia kwamba Elisha alikuwa kule Dotani. Kwa hiyo mufalme akatuma kule kundi kubwa la waaskari pamoja na farasi na magari ya vita. Kundi hilo likafika kule wakati wa usiku na kuuzunguka muji. Mutumishi wa Elisha alipoamuka mapema kesho yake na kutoka inje, akaona waaskari pamoja na farasi na magari ya vita wameuzunguka muji. Akarudi ndani akasema: “Ole wetu, ee, Bwana wangu! Sasa tutafanya nini?” Elisha akamujibu: “Usiogope kwa sababu wanaokuwa pamoja nasi ni wengi kuliko wanaokuwa pamoja nao.” Kisha Elisha akaomba: “Ee Yawe, umufumbue macho kusudi apate kuona!” Basi, Yawe akamufumbua macho yule kijana, akaona farasi na magari ya moto yakiwa kila pahali katika mulima wote, kumuzunguka Elisha. Waaramu waliposhambulia, Elisha alimwomba Yawe akisema: “Ninakuomba ufanye watu hawa wakuwe vipofu!” Yawe akasikiliza ombi lake na kuwafanya vipofu. Halafu Elisha akawaendea na kuwaambia: “Mumepotea njia. Huu siyo muji ambao munautafuta. Munifuate nami nitawapeleka kwa yule munayemutafuta.” Naye akawaongoza mpaka Samaria. Mara tu walipoingia katika muji, Elisha akaomba, akisema: “Ee Yawe, uwafumbue macho kusudi waone.” Yawe akasikia ombi lake, akawafumbua macho. Nao wakajikuta wako katikati ya muji wa Samaria. Mufalme wa Israeli alipowaona Waaramu, alimwuliza Elisha: “Niwaue?” Elisha akajibu: “Hapana, usiwaue. Maana hawa unaotaka kuwaua uliwateka kwa upanga wako na mushale wako? Uwape chakula na maji, wakule na kunywa kisha uwaache warudie kwa bwana wao.” Mufalme wa Israeli akawafanyia karamu kubwa. Walipomaliza kula na kunywa, akawarudisha kwa bwana wao. Toka wakati ule, Waaramu hawakuishambulia tena inchi ya Israeli. Nyuma ya hayo, mufalme Beni-Hadadi wa Aramu akakusanya waaskari wake wote akatoka na kuuzunguka muji wa Samaria. Matokeo yake ilikuwa njaa kali katika muji wa Samaria. Kichwa cha punda kilinunuliwa kwa vikoroti makumi tatu vya feza, na grama mia moja za mavi ya njiwa zilinunuliwa kwa vikoroti vitano vya feza. Siku moja mufalme wa Israeli alipokuwa anatembea juu ya ukuta wa muji, alisikia mwanamuke mumoja akimwita: “Unisaidie, ee bwana wangu mufalme!” Mufalme akamwambia: “Yawe asipokusaidia, mimi nitaweza kukupa musaada kutoka wapi? Kutoka katika kiwanja cha kupepetea ngano au kutoka katika kikamulio? Shida yako ni nini?” Akamujibu: “Juzi mwanamuke huyu alinishauria tumukule mwana wangu na kesho yake tutamukula wake. Tukamupika mwana wangu, tukamukula. Kesho yake nikamwambia tumukule mwana wake, lakini alikuwa amemuficha!” Mara mufalme aliposikia maneno ya mwanamuke yule alipasua nguo zake kwa huzuni, na watu waliokuwa karibu na ukuta waliona kwamba alikuwa amevaa nguo ya gunia ndani yake. Naye akasema: “Mungu aniue Elisha mwana wa Safati asipokatwa kichwa leo!” Halafu akatuma mujumbe kwenda kumuleta Elisha. Wakati uleule, Elisha alikuwa ndani ya nyumba pamoja na wazee waliomutembelea. Mbele ya kufika kwa mujumbe wa mufalme, Elisha akawaambia wazee: “Yule mwuaji amemutuma mutu kuja kunikata kichwa! Atakapofika hapa, mufunge mulango, wala musimuruhusu aingie. Vilevile bwana wake anamufuata nyuma.” Mbele hata hajamaliza kusema, mufalme akafika, akasema: “Mabaya haya yametoka kwa Yawe! Nitangojea nini tena kutoka kwake?” Elisha akamujibu: “Sikiliza neno la Yawe: Kesho kwa wakati kama huu, humu Samaria kilo tatu za unga bora wa ngano zitanunuliwa kwa kipande kimoja cha feza, na kilo sita za shayiri kwa kipande kimoja cha feza.” Jemedari mulinzi wa mufalme akamwambia Elisha: “Hata kama Yawe mwenyewe angefanya madirisha mbinguni, jambo hilo litawezekana?” Elisha akamujibu: “Utaona kwa macho yako mwenyewe, lakini wewe hautakula.” Kulikuwa watu wane wenye ugonjwa wa ukoma waliokuwa inje ya milango ya muji wa Samaria ambao walisemezana, wao kwa wao: “Mbona tunakaa hapa tukikufa na njaa? Hakuna maana ya kuingia katika muji kwa sababu kule tutakufa. Kwa hiyo kumbe tuende kwenye kambi ya Waaramu. Kama wakituacha kuishi, tutaishi; kama wakituua, tutakufa tu.” Hivyo, giza lilipoanza kuingia, wakaenda kwa kambi ya Waaramu, lakini walipofika kule, hakukuwa mutu. Maana Yawe alikuwa amewasikilizisha waaskari wa Waaramu sauti kama ya kundi kubwa lililokuwa na magari na farasi. Waaramu wakazani kwamba mufalme wa Israeli amelipa waaskari wa Wahiti na Wamisri kuja kuwashambulia. Basi, katika usiku ule, Waaramu walikimbia wote kwa kuyaokoa maisha yao wakiacha mahema yao, farasi na punda wao, na hata kambi yao jinsi ilivyokuwa. Wale watu wane wenye ukoma walipofika pembeni ya kambi, waliingia ndani ya hema moja, wakakula na kunywa vile walivyopata mule, wakatwaa feza, zahabu na nguo, wakaenda kuzificha. Wakaingia katika hema ingine na kufanya vivyo hivyo. Lakini wakaambiana: “Tunalofanya si sawa! Hii ni habari njema tunayokuwa nayo leo, na ikiwa tutangoja mpaka asubui, bila shaka tutaazibiwa. Tuende mara moja tuwaambie watu wa nyumba ya mufalme!” Hivyo, wakaondoka katika kambi ya Waaramu na kuwaita walinda milango ya muji na kuwaambia: “Tulikwenda katika kambi ya Waaramu na hatukuweza kumwona wala kumusikia mutu yeyote. Farasi na punda wangali wanafungwa, na mahema yako kama walivyoyaacha.” Walinda milango wakaita mutu mumoja kupasha habari hii katika nyumba ya mufalme. Ingawa kulikuwa bado giza, mufalme aliamuka na kuwaambia wakubwa wa waaskari wake: “Mimi ninajua mupango wa Waaramu! Wanajua tuna njaa katika muji. Sasa wameacha kambi yao kwenda kujificha kusudi tutakapokwenda kutafuta chakula, watukamate wote tungali wazima na kuuteka muji.” Mumoja kati ya wakubwa wake akasema: “Tafazali, utume watu wachache na farasi watano wa wale waliobaki kusudi waende kuona kumetokea nini. Matokeo yao hayatakuwa mabaya zaidi kuliko Waisraeli wote wanaoangamia hapa.” Wakachagua watu na kuwapa magari mawili. Mufalme akawatuma kuwafuata Waaramu, akisema: “Mwende muwaone.” Watu hao wakaenda mpaka Yordani na katika njia waliona nguo na vifaa vingine Waaramu walivyoacha walipokuwa wanakimbia. Wakarudi na kumupasha mufalme habari. Watu wa Samaria wakatoka na kuteka kambi ya Waaramu. Kama vile Yawe alivyosema, kilo tatu za unga bora wa ngano zilinunuliwa kwa kipande kimoja cha feza, na kilo sita za shayiri kwa kipande kimoja cha feza. Naye mufalme alikuwa amemuweka jemadari mulinzi wake kwa kulinda mulango wa muji. Jemadari yule alikanyagwa na watu palepale kwenye mulango, akakufa kama vile Elisha mutu wa Mungu alivyotabiri wakati mufalme alipokwenda kumwona. Elisha alikuwa amemwambia mufalme kwamba “Kesho kwa wakati kama huu, humu Samaria kilo tatu za unga bora wa ngano zitanunuliwa kwa kipande kimoja cha feza, na kilo sita za shayiri kwa kipande kimoja cha feza.” Yule jemedari mulinzi wa mufalme alikuwa amemwambia Elisha: “Hata kama Yawe mwenyewe angefanya madirisha mbinguni, jambo hilo litawezekana?” Naye Elisha alikuwa amemujibu: “Utaona kwa macho yako mwenyewe, lakini wewe hautakula.” Na hivi ndivyo ilivyotokea: alikanyagwa na watu palepale kwenye mulango, akakufa. Elisha alikuwa amemwambia mwanamuke aliyeishi Sunemu ambaye alikuwa amemufufua mwana wake: “Ondoka na jamaa yako, uhamie katika inchi ya kigeni kwa sababu Yawe ameleta njaa itakayokuwa katika inchi kwa muda wa miaka saba.” Yule mwanamuke akaondoka, akafanya kama vile mutu wa Mungu alivyosema. Akaenda pamoja na jamaa yake na kukaa kama mugeni katika inchi ya Wafilistini kwa miaka saba. Miaka saba ilipokwisha, alitoka katika inchi ya Wafilistini akarudi Israeli na kwenda kwa mufalme kuomba arudishiwe nyumba yake na shamba lake. Akamukuta mufalme akiongea na Gehazi, akisema: “Tafazali, uniambie miujiza ambayo inatendwa na Elisha.” Gehazi alipokuwa anamwambia mufalme jinsi Elisha alivyofufua mutu aliyekufa, mwanamuke yule alitoa ombi lake kwa mufalme. Gehazi akasema: “Ee mufalme; huyu ndiye mwanamuke ambaye Elisha alimufufua mwana wake!” Mufalme alipomwuliza mwanamuke yule, yeye alimwelezea. Mufalme akamwita mukubwa wa waaskari wake na kumwamuru amurudishie mwanamuke yule mali yake yote, pamoja na mapato yote ya mashamba yake katika muda ule wote wa miaka saba. Kisha Elisha alikwenda Damasiki. Wakati ule mufalme Beni-Hadadi alikuwa mugonjwa na alipoambiwa kwamba Elisha alikuwa Damasiki, alimwambia Hazaeli mukubwa wa waaskari wake: “Mumupelekee yule mutu wa Mungu zawadi umwambie aombe shauri kwa Yawe kama nitapona au hapana.” Hazaeli akapakia zawadi za kila aina ya mazao ya Damasiki kipimo cha mizigo ya ngamia makumi ine na kumupelekea Elisha. Alipofika kwa Elisha alimwambia: “Mutumishi wako, Beni-Hadadi, mufalme wa Aramu amenituma kwako. Yeye anauliza: ‘Nitapona ugonjwa huu?’ ” Basi Elisha akamujibu: “Umwambie kwamba atapona. Lakini Yawe amenionyesha kwamba atakufa.” Halafu Elisha akamukazia macho hata Hazaeli akashikwa na wasiwasi. Kwa rafla, Elisha mutu wa Mungu akaanza kulia. Hazaeli akamwuliza: “Bwana wangu, mbona unalia?” Elisha akamujibu: “Kwa sababu ninajua maovu ambayo utawatendea watu wa Israeli. Utateketeza kuta zao kwa moto, na kuwaua vijana wao, utawapondaponda watoto wao na kupasua wanawake wenye mimba tumbo.” Hazaeli akauliza: “Lakini mimi mutumishi wako ni kitu kweli? Mimi ninayekuwa sawa na imbwa nitaweza namna gani kutenda mambo hayo makubwa?” Elisha akamujibu: “Yawe amenionyesha kwamba utakuwa mufalme wa Aramu.” Halafu Hazaeli alitoka kwa Elisha, akarudi kwa bwana wake. Mufalme Beni-Hadadi akamwuliza: “Elisha alikuambia nini?” Hazaeli akamujibu: “Aliniambia kwamba hakika utapona.” Lakini kesho yake Hazaeli akatwaa blanketi, akalilowesha ndani ya maji, kisha akamufunika nalo uso mpaka akakufa. Hazaeli akatawala inchi ya Aramu kwa pahali pake. Katika mwaka wa tano wa utawala wa Yoramu mwana wa Ahabu, mufalme wa Israeli, Yehoramu mwana wa Yosafati, mufalme wa Yuda, alianza kutawala. Alipoanza kutawala alikuwa na umri wa miaka makumi tatu na miwili. Alitawala kule Yerusalema miaka minane. Alifuata mwenendo wa wafalme wa Israeli, kama vile jamaa ya Ahabu ilivyofanya, kwa sababu muke wake alikuwa binti ya Ahabu. Akatenda maovu mbele ya Yawe. Lakini Yawe hakutaka kuangamiza Yuda, kwa sababu ya Daudi mutumishi wake, maana aliahidi kwamba wazao wake wataendelea kutawala milele. Wakati wa utawala wa Yehoramu, watu wa Edomu waliasi utawala wa Yuda, wakatawalisha mufalme wao. Kwa hiyo Yoramu aliondoka na magari yake yote kwenda Sairi. Wakati wa usiku alitoka na waongozi wake wa magari akawashambulia Waedomu waliokuwa wamemuzunguka. Lakini waaskari wake walikimbilia kwao. Hivyo watu wa Edomu wakauasi utawala wa Yuda mpaka sasa. Wakati uleule, wakaaji wa Libuna nao wakaasi. Mambo mengine ya Yehoramu na yote aliyofanya yameandikwa katika Kitabu cha Mambo ya Siku za Wafalme wa Yuda. Yehoramu akakufa na kuzikwa katika makaburi ya kifalme katika muji wa Daudi, naye Ahazia mwana wa Yehoramu, akatawala kwa pahali pake. Katika mwaka wa kumi na mbili wa utawala wa Yoramu mwana wa Ahabu mufalme wa Israeli, Ahazia mwana wa Yehoramu mufalme wa Yuda alianza kutawala. Ahazia alianza kutawala akiwa na umri wa miaka makumi mbili na mbili, akatawala akiwa Yerusalema kwa muda wa mwaka mumoja. Mama yake aliitwa Atalia, mujukuu wa mufalme Omuri mufalme wa Israeli. Kwa sababu Ahazia alikuwa mukwe wa jamaa ya Ahabu, naye alifuata mwenendo wa jamaa hiyo ya Ahabu, alitenda maovu mbele ya Yawe, kama vile jamaa ya Ahabu walivyofanya. Mufalme Ahazia akaenda na Yoramu mwana wa Ahabu kupigana vita na Hazaeli mufalme wa Aramu kule Ramoti-Gileadi pahali Waaramu walipomwumizia Yoramu. Kisha mufalme Yoramu akarudi katika muji Yezereheli kusudi apate kutunzwa vidonda alivyoumizwa na Waaramu kule Rama, alipopigana na Hazaeli mufalme wa Aramu. Naye Ahazia mwana wa Yehoramu, mufalme wa Yuda alimwendea Yoramu mwana wa Ahabu kule Yezereheli, kwa sababu alikuwa mugonjwa. Wakati uleule nabii Elisha alimwita mumoja wa wanafunzi wa nabii, akamwambia: “Ujitayarishe kusafiri, twaa chupa hii ya mafuta, na kwenda Ramoti katika Gileadi. Utakapofika kule, umutafute Yehu mwana wa Yosafati, mujukuu wa Nimusi. Umupeleke pembeni ndani ya chumba mbali na wenzake, kisha utwae chupa hii ya mafuta, umumiminie juu ya kichwa na kumwambia: ‘Yawe anasema hivi: Ninakupakaa mafuta ukuwe mufalme wa Israeli.’ Kisha fungua mulango na kuondoka upesi utakavyoweza.” Basi, nabii huyo kijana akaenda Ramoti-Gileadi. Alipofika, aliwakuta wakubwa wa waaskari katika mukutano. Akasema: “Nina ujumbe wako, mukubwa.” Yehu akamwuliza: “Ni nani kati yetu unayemwambia?” Akamujibu: “Wewe, mukubwa.” Halafu wote wawili wakaingia ndani ya chumba cha ndani na kule nabii akamutia Yehu mafuta juu ya kichwa na kumwambia: “Yawe, Mungu wa Israeli, anasema hivi: ‘Ninakupakaa mafuta ukuwe mufalme juu ya watu wangu Israeli. Nawe utaipiga jamaa ya bwana wako Ahabu kusudi nimulipize Yezebeli kisasi kwa damu ya watumishi wangu manabii na ya watumishi wangu wote. Utafanya hivyo kwa sababu jamaa yote ya Ahabu itaangamia. Tena nitamwua kila mwanaume wa jamaa ya Ahabu akuwe mutumwa au mutu huru. Jamaa yake itakuwa kama jamaa ya Yeroboamu mwana wa Nebati na ya Basha mwana wa Ahiya. Yezebeli hatazikwa na mutu. Maiti yake itakuliwa na imbwa katika inchi ya Yezereheli.’ ” Kisha kusema hayo, nabii akaondoka ndani ya chumba na kukimbia. Yehu aliporudi kwa wenzake, mumoja wao alimwuliza: “Kuna shida yoyote? Mwenda-wazimu huyu alitaka nini kwako?” Yehu akawajibu: “Si munamujua yeye na namna yake ya kusema?” Nao wakamwambia: “Hiyo si kweli! Utuambie alilosema!” Akawaambia: “Aliniambia kwamba ‘Yawe anasema hivi: Ninakupakaa mafuta ukuwe mufalme wa Israeli.’ ” Mara moja wakubwa wenzake wakavua nguo zao, wakazilundika pamoja kwenye ngazi kusudi asimame juu yake, wakapiga baragumu na kulalamika kwa sauti: “Yehu ni mufalme!” Yehu mwana wa Yosafati, ambaye vilevile alikuwa mujukuu wa Nimusi, alifanya mupango wa kuasi Yoramu. Yoramu na watu wote wa Israeli walikuwa Ramoti-Gileadi kwa kulinda zamu juu ya mufalme Hazaeli wa Aramu. Lakini mufalme Yoramu alikuwa amerudi Yezereheli kusudi apate kutunzwa vidonda alivyopata wakati wa kupigana katika vita na mufalme Hazaeli wa Aramu. Yehu aliwaambia wakubwa wenzake: “Ikiwa mutakubaliana nami, mutu yeyote asitoke Ramoti kwenda Yezereheli kwa kupeleka habari hizi.” Halafu akapanda ndani ya gari lake na kuelekea Yezereheli. Yoramu alikuwa bado hajapona, na Ahazia mufalme wa Yuda alikuwa amemutembelea. Mulinzi aliyekuwa kwenye zamu juu ya munara wa Yezereheli akasema: “Ninaona watu wakikuja na gari!” Yoramu akajibu: “Chagua askari mupanda-farasi mumoja, umutume kusudi akutane nao, awaulize: ‘Munakuja kwa amani?’ ” Basi, mujumbe huyo alipokwenda alikutana na Yehu na kumwambia: “Mufalme anauliza: unakuja kwa amani?” Yehu akajibu: “Kwa nini unauliza juu ya amani? Wewe geuka ufuatane nami!” Mulinzi juu ya munara akasema: “Mujumbe amewafikia, lakini harudi.” Halafu mujumbe wa pili akatumwa na kumwuliza Yehu: “Mufalme anauliza: unakuja kwa amani?” Yehu akajibu: “Kwa nini unauliza juu ya amani? Wewe geuka ufuatane nami!” Kwa mara ingine tena mulinzi akasema: “Mujumbe amewafikia lakini harudi.” Halafu akaongeza: “Uendeshaji wa gari ni kama wa Yehu mwana wa Nimusi, kwa sababu yeye anaendesha mbiombio.” Basi, Yoramu mufalme wa Israeli akaamuru akisema: “Tayarisha gari.” Nao walitayarisha gari lake. Kisha Yoramu mufalme wa Israeli na Ahazia mufalme wa Yuda waliondoka kila mumoja akipanda ndani ya gari lake, wakaenda kukutana na Yehu. Walimukuta katika uwanja wa Naboti wa Yezereheli. Wakati Yoramu alipomwona Yehu, alimwuliza: “Yehu, unakuja kwa amani?” Yehu akamujibu: “Amani gani, wakati makahaba na wachawi wa Yezebeli ni wengi?” Yoramu aligeuza gari lake na kuondoka, naye akimwambia Ahazia: “Ahazia, huu ni uasi!” Yehu akatwaa upinde wake na kutupa mushale ambao ulipenya mabega ya Yoramu na kuchoma moyo wake, naye akakufa palepale ndani ya gari lake. Yehu akamwambia musaidizi wake Bidikari: “Kamata hiyo maiti yake uitupe katika shamba hilo la Naboti wa Yezereheli. Kwa maana, kumbuka wewe na mimi tulipokuwa tumepanda juu ya farasi wetu nyuma ya baba ya Ahabu, jinsi Yawe alivyosema maneno haya juu yake. Yawe alisema: ‘Kwa ile damu ya Naboti na kwa damu ya wana wake niliyoona jana, nitakulipiza kisasi katika shamba hilo.’ Ni ujumbe wa Yawe. Kwa hiyo, kamata maiti ya Yoramu uitupe katika shamba la Naboti kama vile Yawe alivyosema.” Ahazia mufalme wa Yuda alipoona yaliyotukia alikimbia akielekea Nyumba ya Bustani, naye akifuatwa na Yehu. Yehu akawaamuru watu wake: “Mumwue naye vilevile!” Nao wakamupiga mushale akiwa ndani ya gari kwenye njia ya kupandia Guri karibu na muji wa Ibuleamu. Halafu alikimbilia Megido na kufia kule. Wakubwa wake wakaitwaa maiti yake ndani ya gari lake na kuipeleka Yerusalema. Kule akazikwa katika makaburi ya kifalme katika muji wa Daudi. Ahazia alianza kutawala juu ya Yuda katika mwaka wa kumi na moja wa utawala wa Yoramu mwana wa Ahabu. Yehu alipofika Yezereheli, Yezebeli alikuwa amekwisha kupata habari ya mambo yaliyotokea. Alijipakaa rangi kwenye macho na kuchanua nywele zake, kisha akaenda kwenye dirisha na kuangalia chini. Yehu alipokuwa akiingia kwenye mulango, Yezebeli alisema: “Unakuja kwa amani, ewe Zimuri, wewe unayemwua bwana wako?” Yehu akaangalia juu na kusema: “Ni nani anayekuwa upande wangu?” Wakubwa wawili au watatu wakatokeza vichwa vyao kwa kumwangalia kutoka kwenye dirisha, naye Yehu akawaambia: “Mumutupe chini!” Wakamutupa chini na damu yake ikasambaa juu ya ukuta na kwenye farasi. Yehu akapitisha farasi na gari lake juu ya maiti yake na kuingia katika nyumba ya kifalme, na huko akakula na kunywa. Halafu akaamuru: “Muzike mwanamuke yule aliyelaaniwa kwa sababu ni binti ya mufalme.” Halafu walikwenda kumuzika lakini hawakuona chochote isipokuwa mufupa wa kichwa na mifupa ya mikono na miguu. Kisha walirudi na kumupasha Yehu habari hii, naye akasema: “Hivi ndivyo Yawe alivyotabiri kwa njia ya mutumishi wake Elia wa muji wa Tisibe akisema: ‘Imbwa wataukula mwili wa Yezebeli katika shamba la Yezereheli. Maiti ya Yezebeli itakuwa kama mboleo ndani ya shamba katika inchi ya Yezereheli, hata hakuna atakayeweza kumutambua.’ ” Katika muji wa Samaria kulikuwa wana makumi saba wa Ahabu. Yehu akaandika barua na kutuma barua kwa watawala wa muji, kwa viongozi na kwa walinzi wa wana wa Ahabu. Barua yenyewe ilisema hivi: “Kwa sababu kati yenu kuna wana wa mufalme, vilevile kuna farasi na magari, silaha na miji yenye kuta, muchague na kumuweka mwenye uwezo zaidi kati ya wana wa mufalme kuwa mufalme. Halafu mupigane vita kwa ajili ya ukoo wa mufalme.” Watawala wa Samaria waliogopa sana na kusema: “Tunaweza namna gani kumupiga Yehu wakati mufalme Yoramu na mufalme Ahazia hawakuweza?” Kwa hiyo mukubwa wa nyumba ya mufalme na musimamizi wa muji, wakishirikiana na viongozi wengine na walinzi, wakamupelekea Yehu ujumbe huu: “Sisi ni watumwa wako, na tuko tayari kufanya lolote unalosema. Lakini hatutamuweka mutu yeyote kuwa mufalme. Fanya unavyotaka.” Yehu akawaandikia barua ingine akiwaambia: “Ikiwa kweli muko tayari kufuata maagizo yangu, mulete hapa Yezereheli vichwa vya wana wa bwana wenu nivipate kesho kwa wakati kama huu.” Wana makumi saba wa mufalme Ahabu waliishi kwa viongozi wa Samaria, ambao walikuwa walezi wao. Basi, barua ilipowafikia, waliwatwaa hao wana wa mufalme na kuwakata vichwa wote makumi saba. Waliweka vichwa vyao katika vikapu na kumupelekea Yehu kule Yezereheli. Kisha mutumishi mumoja akamwendea na kusema: “Vichwa vya wana wa mufalme vimekwisha kuletwa.” Halafu akaamuru: “Muviweke chini katika mafungu mawili kwenye mulango wa muji, muviache vikae kule mpaka asubui.” Asubui yake akatoka, akasimama na kuwaambia watu wote: “Ninyi ni watu wa haki. Mimi nilifanya mupango wa kuasi bwana wangu na kumwua. Lakini ni nani aliyewaua hawa wote? Mujue kwamba maneno yote Yawe aliyosema juu ya jamaa ya Ahabu yametimia. Yawe ameyafanya hayo aliyosema kwa njia ya mutumishi wake Elia.” Halafu Yehu akaua jamaa yote ya Ahabu iliyokuwa inakaa Yezereheli, pamoja na wakubwa wake na warafiki na makuhani wake. Hakumwacha hata mutu yeyote. Kisha Yehu aliondoka Yezereheli, akaelekea Samaria. Akiwa katika njia pahali panapoitwa “Kambi ya Wachungaji”, alikutana na watu wa jamaa ya marehemu Ahazia mufalme wa Yuda akawauliza: “Ninyi ni wa nani?” Wakamujibu: “Sisi ni watu wa jamaa ya Ahazia. Tumeteremuka huku kuwatembelea wana wa mufalme na wana wa malkia.” Kisha akaamuru: “Muwakamate wakiwa wazima.” Wakawakamata watu makumi ine na wawili wakawaua karibu na kisima cha “Kambi ya Wachungaji”. Hakuna aliyebaki hata mumoja. Yehu akatoka tena na alipofika katika njia akakutana na Yonadabu mwana wa Rekabu. Yehu akamusalimia, kisha akamwuliza: “Wewe una mawazo sawa na yangu? Utajiunga nami na kunisaidia?” Yonadabu akamujibu: “Ndiyo, nitajiunga nawe.” Yehu akasema: “Basi, unipe mukono wako.” Wakashikana mikono na Yehu akamupandisha ndani ya gari lake. Akamwambia: “Fuatana nami kusudi ujionee jinsi ninavyokuwa mwaminifu kwa Yawe.” Basi, wakasafiri pamoja katika gari lake. Walipofika Samaria, Yehu aliua jamaa yote ya Ahabu bila kumwacha hata mumoja wao, sawa vile Yawe alivyomwambia Elia itakavyokuwa. Yehu akawakusanya watu wa Samaria na kuwaambia: “Mufalme Ahabu alimutumikia Bali kidogo tu, lakini mimi nitamutumikia zaidi. Uwaite manabii wote wa Bali, wafuasi wake wote na makuhani. Ni sharti kila mumoja afike, maana ninataka kumutolea Bali sadaka kubwa, na yeyote atakayekosa kufika atauawa.” Hiyo ilikuwa ni namna ya Yehu ya kudanganya kusudi apate kuwaua wafuasi wa Bali. Yehu akaamuru: “Mutangaze mukutano wa ibada ya Bali!” Tangazo likatolewa, na Yehu akapeleka habari katika inchi yote ya Israeli kusudi wafuasi wote wa Bali wahuzurie kila mumoja. Wakakuja wote na kujaa katika hekalu la Bali kutoka pembe moja mpaka nyingine. Halafu Yehu akamwagiza yule aliyesimamia nguo za ibada hivi: “Ondoa nguo na kuwapa watu wote wanaotumikia Bali.” Musimamizi akatoa nguo zile, akawapa. Halafu Yehu akaingia katika hekalu la Bali akifuatana na Yonadabu na kuwaambia waliokuwa ndani ya hekalu: “Muhakikishe kwamba wanaokuwa humu ndani ya hekalu ni wale wanaomwabudu Bali tu, na kwamba hakuna mutu yeyote anayemwabudu Yawe.” Kisha akaingia pamoja na Yonadabu kwa kumutolea Bali matoleo na sadaka za kuteketezwa. Yehu alikuwa ameweka watu makumi tatu inje ya hekalu na kuwapa maagizo haya: “Muwaue watu hawa wote. Yeyote atakayemwacha hata mumoja wao atoroke atalipa kwa maisha yake!” Mara tu Yehu alipomaliza kutoa sadaka ya kuteketezwa, aliwaambia walinzi na wakubwa: “Muingie muwaue wote. Musimwache hata mumoja atoroke!” Wakaingia na panga zao tayari na kuwaua wote, kisha wakatoa maiti zao inje. Halafu wakaingia katika chumba cha ndani cha hekalu, na kutoa nguzo takatifu na kuiteketeza kwa moto. Wakaharibu nguzo pamoja na hekalu; wakaigeuza hekalu kuwa choo, na hivi ndivyo inavyokuwa mpaka hivi leo. Hivi ndivyo Yehu alivyomaliza ibada za Bali katika Israeli. Lakini hakuacha zambi zile za Yeroboamu mwana wa Nebati ambaye aliwasukuma Waisraeli watende zambi, ni kusema ile ibada ya sanamu za wana-ngombe wa zahabu kule Beteli na Dani. Yawe akamwambia Yehu: “Umewatendea wazao wa Ahabu yale yote niliyotaka uwatendee. Kwa hiyo nimekuahidi kwamba wazao wako mpaka kizazi cha ine watatawala Israeli.” Lakini Yehu hakutii sheria za Yawe, Mungu wa Israeli, kwa moyo wake wote. Hakuacha zambi zile za Yeroboamu ambaye aliwasukuma watu wa Israeli watende zambi. Wakati ule Yawe alianza kupunguza eneo la inchi ya Israeli. Mufalme Hazaeli wa Aramu akashinda inchi yote ya Israeli katika upande wa mashariki ya muto Yordani, na inchi za Gileadi, Gadi, Rubeni na Manase na kutoka muji wa Aroeri unaokuwa kwenye bonde la Arnoni, kwenye inchi za Gileadi na Basani. Mambo mengine ya Yehu, yote aliyofanya na ushujaa wake yameandikwa katika Kitabu cha Mambo ya Siku za Wafalme wa Israeli. Akakufa na kuzikwa Samaria. Mwana wake Yoahazi akatawala kwa pahali pake. Yehu alitawala Israeli akiwa Samaria kwa miaka makumi mbili na minane. Mara tu Atalia mama ya mufalme Ahazia alipoona kwamba mwana wake ameuawa, alitoka, akaangamiza watu wote wa jamaa ya kifalme. Lakini Yoseba binti ya mufalme Yoramu, dada ya Ahazia, alimutwaa kwa siri Yoasi mwana wa Ahazia, kutoka kati ya wana wa mufalme waliokuwa karibu kuuawa. Alimuficha yeye pamoja na mulezi wake katika chumba cha kulala. Hivyo walimuficha kusudi Atalia asimwone na kumwua. Yoasi alikaa naye kwa muda wa miaka sita akiwa amefichwa ndani ya nyumba ya Yawe, wakati Atalia alipokuwa akitawala katika inchi. Lakini katika mwaka wa saba Yehoyada alituma ujumbe na kuwakusanya wakubwa wa waaskari na walinzi. Akaamuru wamufikie katika nyumba ya Yawe, naye akafanya nao mapatano na kuwaapisha humo katika nyumba ya Yawe. Halafu akawaonyesha Yoasi mwana wa mufalme Ahazia. Kisha akatoa amri: “Mutafanya hivi: mutakapokuja kushika zamu siku ya Sabato, sehemu moja ya tatu italinda nyumba ya kifalme, sehemu ingine moja ya tatu itakuwa kwenye mulango wa Suri na sehemu ingine itakuwa kwenye mulango nyuma ya walinzi. Hivi ndivyo mutakavyolinda nyumba ya kifalme kusudi isivunjwe. Yale makundi mawili ambayo yanamaliza zamu yao siku ya Sabato yatashika zamu katika nyumba ya Yawe kwa kumulinda mufalme. Mutamuzunguka mufalme, kila mutu na silaha yake katika mukono na mutu yeyote atakayesubutu kuwakaribia mumwue. Mukae na mufalme, ikiwa anatoka au anaikaa.” Wakubwa walitii amri zote kuhani Yehoyada alizotoa. Kila mukubwa akakamata watu wake wote, wale waliokuwa wamemaliza zamu na wale waliokuwa wanaingia kushika zamu siku ya Sabato, basi wakamwendea kuhani Yehoyada. Kisha kuhani akawapa wakubwa mikuki na ngao zilizokuwa mali ya mufalme Daudi, na ambazo zilikuwa zimewekwa katika nyumba ya Yawe, nao walinzi walisimama kuanzia upande wa kusini wa nyumba mpaka upande wa kaskazini wa nyumba na kuzunguka mazabahu na nyumba kwa kumuzunguka mufalme; kila mutu akiwa ameshika mukuki wake katika mukono. Halafu Yehoyada akamutoa inje mwana wa mufalme, akamuvalisha taji juu ya kichwa, na kumupa maandiko ya sheria. Wakamuweka kuwa mufalme na kumupakaa mafuta. Wakapiga mikono na kusema: “Mufalme aishi milele!” Naye Atalia aliposikia sauti za walinzi pamoja na za watu wengine, aliwaendea wale watu waliokuwa katika nyumba ya Yawe. Alipochungulia akamwona mufalme mupya akisimama karibu na nguzo kwenye kiingilio cha hekalu kama ilivyokuwa desturi nao wakubwa wa waaskari na wapiga baragumu wakiwa pembeni ya mufalme, na wakaaji wote wakishangilia na kupiga baragumu. Basi, akapasua nguo zake na kusema kwa sauti kubwa: “Uasi! Uasi!” Kisha kuhani Yehoyada akaamuru wakubwa wa waaskari akisema: “Mumwondoshe inje katikati ya waaskari, na muue mutu yeyote atakayemufuata.” Kwa sababu kuhani alisema: “Asiuawe katika nyumba ya Yawe.” Basi, wakamukamata, wakamupeleka na kumupitisha kwenye Mulango wa Farasi kuelekea nyumba ya kifalme, naye akauawa kule. Kisha Yehoyada akafanya agano kati ya Yawe na mufalme na watu kwamba watakuwa watu wa Yawe. Vilevile alifanya agano kati ya mufalme na watu. Halafu wakaaji wakaenda kwenye nyumba ya Bali na kuibomoa, wakavunja mazabahu pamoja na sanamu zake, hata wakamwua Matani, kuhani wa Bali mbele ya mazabahu. Kuhani Yehoyada akaweka walinzi kwa kulinda nyumba ya Yawe. Aliwakamata wakubwa wa waaskari, waaskari walinzi na watu wote, nao wakamusindikiza mufalme kutoka nyumba ya Yawe, wakapitia katika mulango wa walinzi mpaka kwenye nyumba ya kifalme. Naye mufalme akakiikalia kiti cha kifalme. Kwa hiyo, watu wote walipata furaha na muji wote ulikuwa mutulivu, nyuma ya Atalia kuuawa kwa upanga katika nyumba ya kifalme. Yoasi alianza kutawala inchi ya Yuda akiwa na umri wa miaka saba. Katika mwaka wa saba wa utawala ya mufalme Yehu wa Israeli, Yoasi alianza kutawala Yuda kule Yerusalema, naye akatawala kwa muda wa miaka makumi ine akiwa kule Yerusalema. Mama yake aliitwa Sibia wa Beri-Seba. Wakati wa maisha yake yote alitenda kwa usawa mbele ya Yawe, kwa sababu kuhani Yehoyada alikuwa akimufundisha. Hata hivyo, nafasi za kuabudu miungu kwenye milima hazikuharibiwa, na watu waliendelea kutambika na kufukiza ubani kule. Lakini hata nyuma ya miaka makumi mbili na mitatu ya utawala wa Yoasi, makuhani walikuwa bado hawajatengeneza hata mabomoko ya nyumba. Kwa hiyo mufalme Yoasi alimwita kuhani Yehoyada na makuhani wengine na kuwauliza: “Mbona hamujatengeneza nyumba? Basi, sasa hamutapokea tena feza kutoka kwa wengine lakini zitaletwa kusudi nyumba itengenezwe.” Makuhani wakakubali wasipokee feza tena kutoka kwa watu. Vilevile hawakukuwa na madaraka ya kutengeneza nyumba ya Yawe. Yehoyada akatwaa sanduku na kutoboa tundu kwenye kifuniko chake, kisha akaliweka kwenye mazabahu upande wa kuume, mutu anapoingia katika nyumba ya Yawe. Nao makuhani waliokuwa wakichunga kwenye mulango waliweka ndani ya sanduku feza zote zilizotolewa katika nyumba ya Yawe. Kila mara walipoona kwamba kuna feza nyingi ndani ya sanduku, mwandishi wa mufalme na Kuhani Mukubwa waliingia na kupima feza yote iliyopatikana katika nyumba ya Yawe. Halafu kisha kuzipima walizitoa kwa wafanyakazi waliosimamia nyumba ya Yawe, nao wakazilipa kwa waseremala na wenye kujenga waliotengeneza nyumba ya Yawe, kwa wajengaji na wenye kuchonga mawe, na zikatumiwa kwa kununua mbao na mawe yaliyochongwa kwa kutengeneza nyumba ya Yawe na kutimiza mahitaji mengine yote ya kazi ya kutengeneza nyumba. Lakini feza zake hazikutumiwa kwa kulipa kazi za kutengeneza mabeseni ya feza, makasi ya kukata tambi za mishumaa, mabakuli, baragumu, wala kwa vyombo vingine vyovyote vya zahabu au vya feza. Zote zilitumiwa kwa kuwalipa wafanyakazi waliozitumia kwa kutengeneza nyumba ya Yawe. Wafanyakazi waliosimamia kazi hii walikuwa waaminifu kabisa. Kwa hiyo hakukuwa lazima ya kuwaomba watoe hesabu ya matumizi ya feza. Feza zilizotolewa kwa sadaka za malipo kwa ajili ya kosa na kwa sadaka za usamehe wa zambi hazikuingizwa katika nyumba ya Yawe. Hizo zilikuwa ni mali ya makuhani. Wakati huo Hazaeli mufalme wa Aramu akaushambulia muji wa Gati na kuuteka. Lakini Hazaeli alipoelekea Yerusalema kusudi aushambulie, Yoasi mufalme wa Yuda alitwaa sadaka zote zilizotakaswa na babu zake wafalme wa Yuda: Yosafati, Yehoramu na Ahazia, na kuongeza zile zake, pamoja na zahabu yote iliyokuwa katika hazina ya nyumba ya Yawe na katika nyumba ya kifalme, akazituma kwa Hazaeli mufalme wa Aramu. Naye Hazaeli akatoka Yerusalema. Mambo mengine ya Yoasi na yote aliyofanya yameandikwa katika Kitabu cha Mambo ya Siku za Wafalme wa Yuda. Wakubwa wa serikali yake wakamwasi, wakamwuia katika uwanja wa Milo kwenye barabara inayoelekea Sila. Waliomwua ni Yozakari mwana wa Simeati na Yozabadi mwana wa Someri watumishi wake. Halafu wakamuzika katika makaburi ya kifalme katika muji wa Daudi. Naye Amazia mwana wake akatawala kwa pahali pake. Katika mwaka wa makumi mbili na tatu wa utawala wa mufalme Yoasi wa Yuda, Yoahazi mwana wa Yehu alianza kutawala Israeli, akaendelea kutawala akiwa kule Samaria kwa muda wa miaka kumi na saba. Alitenda maovu mbele ya Yawe. Alitenda zambi sawa na Yeroboamu mwana wa Nebati ambaye aliwasukuma watu wa Israeli watende zambi. Hakuacha kutenda zambi hii. Yawe alikasirika, akawafanya watu wa Israeli washindwe katika vita mara kwa mara na mufalme Hazaeli wa Aramu na mwana wake Beni-Hadadi. Yoahazi akamusihi Yawe, naye Yawe alipoona jinsi mufalme wa Aramu alivyowatesa watu wa Israeli akasikia maombi yake. Yawe akawapa Waisraeli kiongozi ambaye aliwakomboa kutoka kwa Waaramu. Halafu wakakaa kwa amani kama vile walivyokuwa zamani. Hata hivyo hawakuacha zambi za mufalme Yeroboamu ambaye aliwasukuma watu wa Israeli watende zambi; lakini waliendelea na zambi zao na sanamu ya Ashera ilibakia kule Samaria. Yoahazi hakukuwa na waaskari, lakini alikuwa tu na wapanda-farasi makumi tano, magari kumi na waaskari wa miguu elfu kumi. Hii ilikuwa ni kwa sababu mufalme wa Aramu alikuwa ameyaangamiza makundi ya waaskari ya Israeli na kuyakanyaga chini kama mavumbi. Mambo mengine ya Yoahazi, yote aliyofanya na ushujaa wake yameandikwa katika Kitabu cha Mambo ya Siku za Wafalme wa Israeli. Yoahazi akakufa na kuzikwa kule Samaria, naye mwana wake Yoasi akakuwa mufalme kwa pahali pake. Katika mwaka wa makumi tatu na saba wa utawala wa mufalme Yoasi wa Yuda, Yoasi mwana wa Yoahazi alianza kutawala Israeli akiwa kule Samaria, na akatawala kwa muda wa miaka kumi na sita. Yoasi vilevile alitenda maovu mbele ya Yawe. Hakuacha zambi zile za Yeroboamu mwana wa Nebati ambaye aliwasukuma watu wa Israeli watende zambi. Aliendelea kuzitenda. Mambo mengine ya Yoasi, yote aliyofanya na ushujaa wake katika vita alivyopigana na mufalme Amazia wa Yuda, yameandikwa katika Kitabu cha Mambo ya Siku za Wafalme wa Israeli. Yoasi akakufa na kuzikwa katika makaburi ya kifalme kule Samaria, naye mwana wake Yeroboamu akatawala kwa pahali pake. Nabii Elisha alipata ugonjwa ambao ulimwua. Alipokuwa karibu kufa, mufalme Yehoasi wa Israeli alimutembelea. Alipomufikia Elisha, akalia, akisema: “Baba yangu, baba yangu! Ulikuwa wa lazima kuliko magari ya Israeli na wapanda-farasi wake!” Elisha akamwamuru: “Ulete upinde na mishale!” Yoasi akavileta. Elisha akamwambia ajitayarishe kupiga mishale. Mufalme akajitayarisha na Elisha akaiweka mikono yake juu ya mikono ya mufalme. Mufalme alifuata maagizo ya nabii na kufungua dirisha ambalo lilielekea Aramu. Elisha akatoa amri: “Tupa mushale!” Mara tu mufalme alipotupa mushale, nabii akasema: “Wewe ndio mushale wa Yawe, ambao kwa njia yake atapata ushindi juu ya Waaramu. Utapigana na Waaramu kule Afeki mpaka uwashinde.” Halafu Elisha akamwambia mufalme atwae mishale mingine na kuipiga chini. Mufalme akapiga mishale chini mara tatu, kisha akaacha. Elisha akakasirika sana, akamwambia mufalme: “Mbona haukupiga mara tano au sita? Hivyo ungewaangamiza Waaramu kabisa. Lakini sasa utawashinda mara tatu tu.” Elisha akakufa, naye akazikwa. Kila mwaka, makundi ya Wamoabu yalikuja kuishambulia inchi ya watu wa Israeli. Siku moja, wakati wa mazishi, watu waliona moja kati ya makundi yale. Wakatupa maiti katika kaburi la Elisha na kukimbia. Mara tu maiti hiyo ilipogusa mifupa ya Elisha, ilifufuka na kusimama wima. Mufalme Hazaeli wa Aramu akawatesa sana watu wa Israeli wakati wote wa utawala wa Yoahazi. Lakini Yawe aliwarehemu na kuwaonea huruma. Aliwaangalia kwa wema kwa sababu ya agano lake na Abrahamu, Isaka na Yakobo. Hakuwaangamiza wala hajawaachilia hata kidogo mpaka leo. Hazaeli mufalme wa Aramu alipokufa, Beni-Hadadi mwana wake akatawala kwa pahali pake. Mufalme Yoasi akamushinda Beni-Hadadi mara tatu na kuikomboa miji yote iliyotekwa wakati wa utawala wa Yoahazi, baba ya Yoasi. Katika mwaka wa pili wa utawala wa Yoasi mwana wa Yoahazi katika inchi ya Israeli, Amazia mwana wa Yoasi mufalme wa Yuda akaanza kutawala. Alipoanza kutawala alikuwa na umri wa miaka makumi mbili na mitano, naye akatawala akiwa Yerusalema kwa muda wa miaka makumi mbili na tisa. Mama yake aliitwa Yoadani wa Yerusalema. Alitenda kwa usawa mbele ya Yawe, lakini hakukuwa kama babu yake Daudi. Akafanya mambo yote kama vile baba yake Yoasi. Nafasi za kutambikia kwenye milima hazikuharibiwa na watu waliendelea kutambika na kufukiza ubani kwa nafasi zile. Wakati Amazia alipojiimarisha katika mamlaka, aliwaua watumishi waliomwua mufalme baba yake. Lakini hakuwaua watoto wa wauaji kama vile ilivyoandikwa katika kitabu cha Sheria ya Musa, Yawe alipotoa amri akisema: “Wazazi hawatauawa kwa ajili ya watoto wao, wala watoto hawatauawa kwa ajili ya wazazi wao; lakini kila mutu atauawa kwa ajili ya zambi zake mwenyewe.” Amazia aliwaua Waedomu elfu kumi katika Bonde la Chumvi. Aliutwaa kwa nguvu muji wa Sela na kuuita Yokiteli, na hivi ndivyo unavyoitwa mpaka sasa. Kisha Amazia akatuma wajumbe kwa Yoasi mwana wa Yoahazi, mujukuu wa Yehu, mufalme wa Israeli akisema: “Ukuje tupigane.” Lakini Yoasi mufalme wa Israeli akamupelekea Amazia mufalme wa Israeli ujumbe, akisema: “Siku moja muti wa mubaruti wa Lebanoni uliuambia muti wa mwerezi wa kule Lebanoni: ‘Umwoeshe binti yako kwa mwana wangu.’ Lakini nyama wa pori akapita pale na kuukanyagakanyaga mubaruti ule. Sasa, wewe Amazia umewashinda kabisa Waedomu, na moyo wako unakufanya ujivune. Ufurahie utukufu wako, ukae katika nyumba yako; kwa nini kujitafutia taabu zitakazokuangamiza wewe mwenyewe pamoja na watu wako wa Yuda?” Lakini Amazia hakujali. Kwa hiyo Yoasi mufalme wa Israeli akatoka akaonana uso kwa uso na Amazia kule katika vita Beti-Semesi, katika inchi ya Yuda. Watu wa Yuda walishindwa na watu wa Israeli na kila mumoja alirudi kwake. Yoasi mufalme wa Israeli alimuteka Amazia mufalme wa Yuda mwana wa Yoasi mwana wa Ahazia kule Beti-Semesi. Halafu akauendea Yerusalema na kuubomoa ukuta wake kutoka kwenye Mulango wa Efuraimu mpaka kwenye Mulango wa Pembeni, umbali wa karibu metre mia mbili. Alitwaa zahabu yote na feza, hata na vifaa vyote vilivyokuwa katika nyumba ya Yawe na katika hazina ya nyumba ya kifalme. Vilevile alibeba mateka, kisha akarudi Samaria. Matendo mengine yote ya Yoasi, ushujaa wake na vita alivyopigana na mufalme Amazia wa Yuda yameandikwa katika Kitabu cha Mambo ya Siku za Wafalme wa Israeli. Yoasi akakufa, akazikwa katika makaburi ya kifalme kule Samaria. Mwana wake, Yeroboamu akatawala kwa pahali pake. Amazia mwana wa Yoasi mufalme wa Yuda aliishi miaka kumi na mitano nyuma ya kufa kwa mufalme Yehoasi wa Israeli mwana wa Yoahazi. Matendo mengine yote ya Amazia yameandikwa katika Kitabu cha Mambo ya Siku za Wafalme wa Yuda. Mupango wa kumwua Amazia ulifanyika Yerusalema. Kwa hiyo akakimbilia Lakisi, lakini waadui walituma watu wa kumwua kule. Maiti yake ililetwa juu ya farasi na kuzikwa katika makaburi ya kifalme katika Yerusalema katika muji wa Daudi. Kisha watu wote wa Yuda wakamukamata Azaria akiwa na umri wa miaka kumi na sita, wakamufanya kuwa mufalme kwa pahali pa Amazia baba yake. Nyuma ya kifo cha baba yake, Azaria akaujenga upya muji wa Elati na kuurudisha kwa Yuda. Katika mwaka wa kumi na tano wa utawala wa Amazia mwana wa Yoasi, mufalme wa Yuda, Yeroboamu mwana wa Yoasi, mufalme wa Israeli, akaanza kutawala akiwa kule Samaria, na akatawala kwa muda wa miaka makumi ine na mumoja. Alitenda maovu mbele ya Yawe; hakuacha zile zambi zote za Yeroboamu mwana wa Nebati ambaye aliwasukuma watu wa Israeli watende zambi. Aliikomboa inchi yote iliyokuwa mali ya Israeli, kutokea Pito la Hamati mpaka bahari ya Chumvi. Hivi ndivyo Yawe alivyoahidi kwa njia ya mutumishi wake Yona mwana wa Amitai, nabii kutoka Gati-Heferi. Ni kwa sababu Yawe aliona taabu kubwa Waisraeli waliyopata maana hakukuwa mutu yeyote wa kuwasaidia. Lakini Yawe hakukuwa amesema kwamba ataangamiza inchi ya Israeli kabisa, halafu akawaokoa kwa njia ya mufalme Yeroboamu mwana wa Yoasi. Mambo mengine ya Yeroboamu, yote aliyofanya, vita alivyopigana kwa ushujaa, na jinsi alivyoikomboa Damasiki na Hamati na kuifanya mali ya Israeli, yote yameandikwa katika Kitabu cha Mambo ya Siku za Wafalme wa Israeli. Yeroboamu akakufa na kuzikwa katika makaburi ya kifalme na mwana wake Zakaria akatawala kwa pahali pake. Katika mwaka wa makumi mbili na saba wa kutawala kwa Yeroboamu mufalme wa Israeli, Azaria mwana wa Amazia, mufalme wa Yuda, akaanza kutawala. Alikuwa na umri wa miaka kumi na sita alipoanza kutawala. Alitawala kwa muda wa miaka makumi tano na miwili akiwa kule Yerusalema. Mama yake aliitwa Yekolia wa Yerusalema. Alitenda kwa usawa mbele ya Yawe kama vile baba yake Amazia alivyotenda. Hata hivyo, nafasi za kutambikia kwenye milima hazikuharibiwa, na watu waliendelea kutambika na kufukiza ubani pale. Yawe akamwazibu Azaria, akakuwa na ukoma mpaka alipokufa. Alikaa katika nyumba ya pekee na shuguli zake zote za utawala ziliendeshwa na mwana wake Yotamu. Mambo mengine ya Azaria na yote aliyofanya yameandikwa katika Kitabu cha Mambo ya Siku za Wafalme wa Yuda. Azaria akakufa na kuzikwa katika makaburi ya wafalme katika muji wa Daudi; na mwana wake Yotamu akatawala kwa pahali pake. Katika mwaka wa makumi tatu na nane wa utawala wa Azaria mufalme wa Yuda, Zakaria mwana wa Yeroboamu akaanza kutawala Israeli. Akatawala kwa muda wa miezi sita. Naye, kama vile watangulizi wake, alitenda maovu mbele ya Yawe; hakuacha zambi zile za Yeroboamu mwana wa Nebati ambaye aliwasukuma watu wa Israeli watende zambi. Salumu mwana wa Yabesi alimwasi, akamupiga mbele ya watu na kumwua, kisha akatawala kwa pahali pake. Matendo mengine yote ya Zakaria yameandikwa katika Kitabu cha Mambo ya Siku za Wafalme wa Israeli. Basi tukio hilo lilitokana na ahadi ya Yawe kwa mufalme Yehu, kusema: “Wazao wako watatawala Israeli mpaka kizazi cha ine.” Katika mwaka wa makumi tatu na tisa wa utawala wa mufalme Azaria wa Yuda, Salumu mwana wa Yabesi akaanza kutawala Israeli na akatawala akiwa kule Samaria kwa muda wa mwezi mumoja. Menahemu mwana wa Gadi aliondoka Tirza kwenda Samaria, na kule akamupiga Salumu mwana wa Yabesi, kisha akatawala kwa pahali pake. Matendo mengine yote ya Salumu na uasi wake, yameandikwa katika Kitabu cha Mambo ya Siku za Wafalme wa Israeli. Menahemu alipokuwa katika njia kutoka Tirza, aliuharibu kabisa muji wa Tapua na kuangamiza wakaaji wake pamoja na inchi yote iliyouzunguka kwa sababu hawakujitoa kwake. Vilevile akapasua tumbo za wanawake wenye mimba. Katika mwaka wa makumi tatu na tisa wa utawala wa mufalme Azaria wa Yuda, Menahemu mwana wa Gadi akaanza kutawala Israeli. Akatawala akiwa kule Samaria kwa muda wa miaka kumi. Alitenda maovu mbele ya Yawe. Hakuacha maovu ya Yeroboamu mwana wa Nebati, ambaye aliwasukuma watu wa Israeli watende zambi. Basi, Puli mufalme wa Asuria akashambulia inchi ya Israeli, naye Menahemu akamupa kilo elfu makumi tatu na ine za feza kusudi amusaidie kuimarisha mamlaka yake juu ya inchi ya Israeli. Menahemu alipata feza hiyo kwa kuwalazimisha watajiri wa Israeli kutoa muchango wa vikoroti makumi tano vya feza kila mumoja. Halafu Puli hakukaa Israeli lakini akarudi katika inchi yake. Mambo mengine ya Menahemu na yote aliyofanya yameandikwa katika Kitabu cha Mambo ya Siku za Wafalme wa Israeli. Menahemu akakufa, naye mwana wake Pekahia akatawala kwa pahali pake. Katika mwaka wa makumi tano wa utawala wa mufalme Azaria wa Yuda, Pekahia mwana wa Menahemu akaanza kutawala Israeli. Akatawala akiwa kule Samaria kwa muda wa miaka miwili. Alitenda maovu mbele ya Yawe; hakuacha zambi za Yeroboamu mwana wa Nebati ambaye aliwasukuma watu wa Israeli watende zambi. Peka mwana wa Remalia, ambaye alikuwa mukubwa wa waaskari wa Pekahia, alishirikiana na watu wengine makumi tano kutoka Gileadi, akamwua Pekahia katika chumba cha ndani cha nyumba ya mufalme kule Samaria na kuwa mufalme kwa pahali pake. Mambo mengine ya Pekahia na yote aliyofanya yameandikwa katika Kitabu cha Mambo ya Siku za Wafalme wa Israeli. Katika mwaka wa makumi tano na mbili wa utawala wa mufalme Azaria wa Yuda, Peka mwana wa Remalia akaanza kutawala akiwa kule Samaria kwa muda wa miaka makumi mbili. Alitenda maovu mbele ya Yawe; hakuacha zambi za Yeroboamu mwana wa Nebati ambaye aliwasukuma watu wa Israeli watende zambi. Wakati wa utawala wa Peka mufalme wa Israeli, Tigilati-Pileseri, mufalme wa Asuria, aliteka miji ya Iyoni, Abeli-Beti-Maka, Yanoa, Kadesi na Hazori, pamoja na inchi za Gileadi, Galilaya na Nafutali na kuwahamisha wakaaji wake kwenda Asuria. Katika mwaka wa makumi mbili wa utawala wa Yotamu mwana wa Uzia mufalme wa Yuda, Hoshea mwana wa Ela alimwasi Peka mwana wa Remalia na kumwua, kisha akatawala kwa pahali pake. Mambo mengine ya Peka na yote aliyoyafanya yameandikwa katika Kitabu cha Mambo ya Siku za Wafalme wa Israeli. Katika mwaka wa pili wa utawala wa Peka mwana wa Remalia katika inchi ya Israeli, Yotamu mwana wa Uzia, mufalme wa Yuda, akaanza kutawala Yuda. Alikuwa na umri wa miaka makumi mbili na mitano alipoanza kutawala, akatawala akiwa kule Yerusalema kwa muda wa miaka kumi na sita. Mama yake aliitwa Yerusa, binti ya Zadoki. Yotamu alitenda kwa usawa mbele ya Yawe kama vile baba yake Uzia alivyotenda. Hata hivyo, nafasi za kutambikia miungu ya uongo hazikuharibiwa, na watu waliendelea kutambikia na kufukiza ubani kwenye nafasi za juu. Yotamu alijenga mulango wa kaskazini wa nyumba ya Yawe. Mambo mengine ya Yotamu na yote aliyofanya yameandikwa katika Kitabu cha Mambo ya Siku za Wafalme wa Yuda. Wakati wa utawala wa Yotamu, Yawe akaanza kutuma mufalme Resini wa Aramu na mufalme Peka wa Israeli kwa kushambulia inchi ya Yuda. Yotamu akakufa na kuzikwa katika makaburi ya kifalme katika muji wa Daudi. Mwana wake Ahazi akatawala kwa pahali pake. Katika mwaka wa kumi na saba wa utawala wa Peka mwana wa Remalia, mufalme wa Israeli, Ahazi mwana wa Yotamu, mufalme wa Yuda, akaanza kutawala. Alikuwa na umri wa miaka makumi mbili alipoanza kutawala. Akatawala kwa muda wa miaka kumi na sita akiwa kule Yerusalema. Hakutenda kwa usawa mbele ya Yawe kama vile Daudi babu yake alivyofanya, lakini alifuata mwenendo wa wafalme wa Israeli. Akamutambikia hata mwana wake kwa kuteketezwa kwa moto, akifuata desturi mbaya za mataifa ambayo yalifukuzwa na Yawe wakati Waisraeli walipokuwa wanaingia katika inchi. Ahazi alitambikia sadaka na kufukiza ubani kwenye nafasi yenye kuinuka, juu ya vilima na chini ya kila muti wenye majani mengi. Kisha Resini mufalme wa Aramu na Peka mwana wa Remalia mufalme wa Israeli walitokea kwa kupiga vita na Yerusalema, nao waliuzunguka, lakini hawakuweza kuuteka. Wakati ule, mufalme wa Edomu aliuteka akawarudishia Waedomu muji wa Elati na kuwafukuza watu wa Yuda waliokaa mule. Nao Waedomu wakaingia Elati na kufanya makao yao kule mpaka sasa. Basi Ahazi akatuma watu kwa mufalme Tigilati-Pileseri wa Asuria wakiwa na ujumbe huu: “Mimi ni mutumishi wako mwaminifu. Ukuje uniokoe kutoka kwa wafalme wa Aramu na Israeli ambao wananishambulia.” Ahazi akatwaa feza na zahabu iliyokuwa katika nyumba ya Yawe na hazina iliyokuwa katika nyumba ya mufalme na kumupelekea kama zawadi mufalme wa Asuria. Tigilati-Pileseri, akiitika kwa ombi la Ahazi, aliushambulia muji wa Damasiki na kuuteka. Akamwua mufalme Resini na kuwapeleka wafungwa kule Kiri. Mufalme Ahazi alipokwenda Damasiki kukutana na mufalme Tigilati-Pileseri, aliona mazabahu kule. Basi, akamutumia kuhani Uria mufano kamili na muchoro wa mazabahu hiyo. Uria akajenga mazabahu ile kulingana na mufano ule na kuimaliza mbele ya kurudi kwa Ahazi. Ahazi aliporudi kutoka Damasiki, aliiona mazabahu ile; basi akaikaribia mazabahu na kutoa sadaka juu yake. Alitolea sadaka yake ya kuteketezwa, ya ngano, na ya kinywaji, akanyunyiza damu ya sadaka ya amani. Mazabahu ya shaba ambayo ilitakaswa kwa ajili ya Yawe, aliiondoa mbele ya nyumba kutoka nafasi yake katikati ya mazabahu yake na nyumba ya Yawe, akaiweka kwenye nafasi iliyokuwa upande wa kaskazini wa mazabahu yake. Kisha alimwamuru Uria: “Tumia hii mazabahu yangu kubwa kwa kuteketeza sadaka za asubui na sadaka za unga za magaribi, sadaka za kuteketezwa, sadaka za unga za mufalme na za watu wote na vilevile sadaka za divai za watu. Unyunyize damu ya nyama wote wa kuteketezwa ambao wametolewa sadaka. Lakini ile mazabahu ya shaba nitaitumia mimi kwa kuuliza shauri toka kwa Mungu.” Naye Uria akafuata maagizo ya mufalme. Mufalme Ahazi aliviondoa vile vishikio vilivyokuwa vikisimamishwa kule, akaondoa na bakuli lake ambalo lilikuwa juu ya wale ngombe dume kumi na wawili wa shaba na kuliweka juu ya musingi wa mawe. Nalo baraza la Sabato lililokuwa limejengwa ndani ya nyumba pamoja na mulango wa inje, mufalme alivihamisha kutoka katika nyumba ya Yawe kwa ajili ya mufalme wa Aramu. Matendo mengine yote ya mufalme Ahazi yameandikwa katika Kitabu cha Mambo ya Siku za Wafalme wa Yuda. Ahazi akakufa na kuzikwa katika makaburi ya kifalme katika muji wa Daudi, naye mwana wake Hezekia akatawala kwa pahali pake. Katika mwaka wa kumi na mbili wa utawala wa mufalme Ahazi wa Yuda, Hoshea mwana wa Ela akaanza kutawala Israeli, na utawala wake uliendelea ukiwa kule Samaria kwa miaka tisa. Alitenda maovu mbele ya Yawe ingawa siyo kama wafalme wa Israeli waliomutangulia. Mufalme Salmanaseri wa Asuria alimushambulia; naye Hoshea akakuwa mutumishi wake na kumulipa kodi. Lakini wakati mumoja Hoshea alituma wajumbe kwa mufalme wa Misri akiomba musaada; ndipo akaacha kulipa kodi kwa mufalme Salmanaseri wa Asuria kama vile alivyozoea kufanya kila mwaka. Salmanaseri alipoona hivi alimufunga Hoshea kwa minyororo na kumuweka katika kifungo. Kisha mufalme wa Asuria akashambulia inchi nzima na kuufikia muji wa Samaria na kuuzunguka kwa muda wa miaka mitatu. Katika mwaka wa tisa wa utawala wa Hoshea, mufalme wa Asuria aliuteka muji wa Samaria na kuwapeleka watu wa Israeli katika uhamisho mpaka Asuria. Wamoja kati yao akawaweka katika muji wa Hala, wengine karibu na muto Habori, muto Gozani na wengine katika miji ya Wamedi. Haya yote yalitendeka kwa sababu watu wa Israeli walimwasi Yawe, Mungu wao, ambaye aliwatoa kutoka mikono ya mufalme wa Misri, vilevile waliabudu miungu mingine, na kufuata njia za mataifa ambayo Yawe aliyafukuza wakati watu wake walipokuwa wanaingia, na kufanya matendo ya wafalme wa Israeli waliyoyaingiza katika inchi. Watu wa Israeli walitenda kwa siri mambo yasiyokuwa mema mbele za Yawe, Mungu wao. Walijenga nafasi ya kuabudu miungu ya uongo katika kila muji, kuanzia kwenye munara wa walinzi katika mashamba mpaka katika miji yenye kuta. Juu ya kila kilima na chini ya kila muti wenye majani mabichi, walijenga nguzo za mawe na sanamu za miungu wa kike Ashera, na wakafukiza ubani kwenye mazabahu yote ya miungu ya uongo kwa kufuata desturi za mataifa ambayo yalifukuzwa na Yawe. Walimukasirikisha Yawe na matendo yao maovu, na walitumikia sanamu ambazo Yawe alikuwa amewakataza, akisema: “Musifanye hivyo.” Yawe alituma manabii na waonaji kuionya inchi ya Israeli na ya Yuda akisema: “Mwache njia zenu mbaya mutii amri zangu na masharti yangu kufuatana na sheria nilizowapa babu zenu, na ambazo niliwapa ninyi kupitia kwa watumishi wangu manabii.” Lakini wao hawakutii; walikuwa wagumu kama babu zao ambao hawakumwamini Yawe, Mungu wao. Walikataa kutii masharti yake; hawakushika agano alilofanya na babu zao, walizarau maonyo yake, waliabudu sanamu zisizokuwa na maana hata wao wenyewe hawakukuwa na maana tena, walifuata desturi za mataifa yaliyowazunguka: walizarau amri za Yawe; wala hawakuzishika. Walivunja amri zote za Yawe, Mungu wao. Wakatengeneza sanamu za miungu ya wana-ngombe wawili wa madini yenye kuyeyushwa, wakatengeneza sanamu za Ashera, wakaabudu jeshi la mbingu, na wakamutumikia Bali. Waliwatambikia watoto wao wa kiume na wa kike kwa miungu ya uongo; wakaomba shauri kwa watabiri na wachawi. Walijitoa kabisa kutenda maovu mbele ya Yawe, wakamukasirikisha sana. Basi, Yawe akawakasirikia sana watu wa Israeli na kuwafukuza kabisa mbele yake; hakuacha mutu isipokuwa kabila la Yuda peke yake. Lakini hata watu wa Yuda hawakutii amri za Yawe, Mungu wao; lakini walifuata desturi zilizoletwa na watu wa Israeli. Yawe aliwakataa Waisraeli wote; akawaazibu na kuwaacha katika mikono ya waadui wakali, na kisha akawafukuza mbele yake. Nyuma ya Yawe kutenga Israeli kutoka ukoo wa Daudi walimuweka Yeroboamu mwana wa Nebati kuwa mufalme. Naye Yeroboamu aliwasukuma watu wa Israeli kumwacha Yawe na kutenda zambi kubwa sana. Waisraeli walitenda zambi zote Yeroboamu alizotenda. Hawakuziacha mpaka kwa mwisho Yawe akawafukuza kutoka mbele yake, kama vile alivyokuwa amesema kupitia kwa watumishi wake wote manabii. Kwa hiyo watu wa Israeli walipelekwa katika uhamisho kutoka katika inchi yao wenyewe mpaka Asuria ambako wanakaa hata sasa. Kisha mufalme wa Asuria akapeleka watu kutoka Babeli, Kuta, Awa, Hamati na Sefarwaimu na kuwaweka katika miji ya Samaria kwa pahali pa watu wa Israeli waliopelekwa katika uhamisho. Wakaitwaa miji hiyo na kukaa mule. Basi ikatokea kwamba walipoanza kukaa mule, hawakumwabudu Yawe, kwa hiyo Yawe akatuma simba kati yao, nao wakawaua wamoja kati yao. Halafu watu wakamwambia mufalme wa Asuria, “Mataifa uliyoyakamata na kuyaweka katika miji ya Samaria hayakujua hukumu za Mungu wa inchi hiyo, kwa hiyo Mungu huyo alituma simba ambao wanawaua.” Halafu mufalme wa Asuria akaamuru: “Murudishe kuhani mumoja kati ya wale tuliowaleta katika uhamisho. Mumurudishe aende na kukaa kule, kusudi awafundishe watu sheria ya Mungu wa inchi hiyo.” Kwa hiyo, mumoja wa makuhani waliopelekwa katika uhamisho toka Samaria alikwenda na kukaa Beteli, na kule akawafundisha watu jinsi ya kumwabudu Yawe. Lakini mataifa yote katika miji yalimoishi yalijitengenezea miungu yao na kuiweka kwa nafasi zenye kuinuka ambako watu wa Samaria walikuwa wametengeneza. Watu wa Babeli walitengeneza sanamu za Sukoti-Benoti, watu wa Kuta wakatengeneza sanamu za Nergali, watu wa Hamati sanamu za Asima, watu wa Awa sanamu za Nibunasi na za Tartaki, na Wasefarwaimu walitoa watoto wao kuwa sadaka za kuteketezwa kwa miungu yao Adarameleki na Anameleki. Watu hawa vilevile walimwabudu Yawe. Walichagua kutoka kati yao watu wa kila aina na kuwafanya makuhani kutumika katika nafasi zenye kuinuka juu na kutoa sadaka kule kwa ajili yao. Hivi wakamwabudu Yawe, lakini wakati uleule wakiwaabudu vilevile miungu yao waliyoleta kutoka inchi zao. Hata sasa wanatenda kama vile walivyofanya zamani. Hawamwabudu Yawe, wala hawafuati masharti, maagizo, sheria au amri ambazo yeye Yawe aliwaamuru wana wa Yakobo; ambaye alimupa jina la Israeli. Yawe alikuwa amefanya agano nao na kuwaamuru: “Musiabudu miungu mingine; musiiname mbele yake, musiitumikie wala musiitambikie. Mutaniabudu mimi Yawe, ambaye niliwatoa kule Misri kwa uwezo na nguvu nyingi. Mutainama mbele yangu mimi na kunitolea sadaka. Wakati wote mutatii masharti, maagizo, sheria na amri ambazo niliandika kwa ajili yenu, siku zote mutakuwa waangalifu kwa kuzitenda. Musiiabudu miungu mingine, wala musisahau agano nililofanya nanyi, musiiabudu miungu mingine, lakini mutaniabudu mimi Yawe, Mungu wenu, nami nitawaokoa kutoka katika mikono ya waadui zenu.” Lakini watu hao hawakusikiliza, wao waliendelea kutenda kama vile walivyofanya zamani. Basi mataifa haya yalimwabudu Yawe, lakini vilevile walitumikia sanamu zao za madini yenye kuyeyushwa; na mpaka sasa hivi, wazao wao wanaendelea kutenda hivyo kama vile babu zao walivyotenda. Katika mwaka wa tatu wa utawala ya Hoshea mwana wa Ela, mufalme wa Israeli, Hezekia mwana wa Ahazia, mufalme wa Yuda, alianza kutawala. Alikuwa na umri wa miaka makumi mbili na mitano alipoanza kutawala. Akatawala miaka makumi mbili na tisa akiwa kule Yerusalema. Mama yake aliitwa Abi binti ya Zakaria. Alitenda kwa usawa mbele ya Yawe, kama vile Daudi babu yake alivyotenda. Aliharibu nafasi zote za kuabudu miungu na kuvunja nguzo na kukata Ashera. Vilevile, alivunja nyoka ya shaba ambayo Musa alitengeneza, iliyoitwa Nehustani. Mpaka wakati ule, watu wa Israeli walikuwa wakiitambikia. Hezekia alimutegemea Yawe, Mungu wa Israeli; hakuna aliyekuwa kama yeye kati ya wafalme wa Yuda waliomufuata au waliomutangulia. Yeye hakumwasi Yawe wala hakuacha kumufuata, lakini alishika amri ambazo Yawe alimupa Musa. Basi, Yawe alikuwa pamoja naye, na alimwezesha kwa kila jambo alilotenda. Alimwasi mufalme wa Asuria na kukataa kumutumikia. Aliwapiga Wafilistini mpaka muji wa Gaza na inchi iliyouzunguka, kuanzia kwenye munara wa walinzi mpaka muji wenye kuta. Katika mwaka wa ine wa utawala wa Hezekia, ambao vilevile ulikuwa mwaka wa saba wa utawala wa Hoshea mwana wa Ela mufalme wa Israeli, Salmanaseri mufalme wa Asuria alishambulia muji wa Samaria na kuuzunguka. Kwa mwisho wa mwaka wa tatu Waasuria waliuteka muji wa Samaria. Ilikuwa katika mwaka wa sita wa utawala wa Hezekia na vilevile mwaka wa tisa wa utawala wa Hoshea mufalme wa Israeli, muji wa Samaria ulipotekwa. Mufalme wa Asuria akakamata watu wa Israeli na kuwapeleka mpaka Asuria na kuwaweka wengine wao katika muji wa Hala, na karibu ya Habori, muji wa Gozani, vilevile na wengine katika miji ya Wamedi, kwa sababu Waisraeli hawakutii sauti ya Yawe, Mungu wao, lakini walivunja agano lake, hata hawakusikia wala kutii yote Musa, mutumishi wa Yawe, aliyowaamuru. Katika mwaka wa kumi na ine wa utawala wa mufalme Hezekia, mufalme Saniharibu wa Asuria aliishambulia miji yote yenye kuta ya Yuda na kuiteka. Hezekia akatuma ujumbe kwa Saniharibu kule Lakisi na kumwambia: “Nimefanya makosa. Tafazali, uache kunishambulia, nami nitalipa chochote unachotaka.” Mufalme wa Asuria akaagiza Hezekia amuletee kilo elfu kumi za feza na kilo elfu moja ya zahabu. Hezekia akamupelekea feza yote iliyokuwa katika nyumba ya Yawe na katika hazina za nyumba ya mufalme. Vilevile, akaondoa zahabu kutoka katika milango ya hekalu la Yawe na ile zahabu ambayo yeye mwenyewe aliiweka kwenye miimo ya mulango. Yote akamupelekea Saniharibu. Kisha mufalme wa Asuria alimutuma majemadari wakubwa watatu pamoja na kundi kubwa la waaskari kutoka Lakisi kwenda kwa mufalme Hezekia kule Yerusalema. Walisafiri na kufika Yerusalema. Nao walipofika waliingia na kusimama karibu na mufereji wa kisima kinachokuwa upande wa juu katika barabara kubwa inayoelekea kiwanja cha mufuaji wa nguo. Walipomwita mufalme Hezekia walipokelewa na Eliakimu mwana wa Hilkia ambaye alikuwa musimamizi wa nyumba ya kifalme, Sebuna aliyekuwa mwandishi wa mufalme, na Yoa mwana wa Asafu, mwandishi wa habari. Mumoja wa wale majemadari wakubwa akawaambia: “Mumwambie Hezekia kwamba mufalme mukubwa wa Asuria anamwuliza: Unategemea nini kwa kukazana kwako? Unazani kwamba maneno matupu ndiyo maarifa na nguvu katika vita? Ni nani unayemutegemea hata ukaniasi? Angalia sasa. Unategemea Misri, utete uliovunjika ambao utamuchoma mukono mutu yeyote atakayeutegemea. Hivi ndivyo mufalme wa Misri anavyokuwa kwa wote wale wanaomutegemea. Lakini hata kama mukiniambia: ‘Tunamutegemea Yawe, Mungu wetu’, si huyohuyo ambaye Hezekia aliziharibu nafasi zake zote za kuabudu kwenye vilima pamoja na mazabahu zake na kuwaambia watu wa Yuda na Yerusalema: Munapaswa kuabudu mbele ya mazabahu hii ya Yerusalema tu? Basi, mufanye mapatano na bwana wangu mufalme wa Asuria. Mimi nitawapatia farasi elfu mbili, kama mutaweza kupata waaskari wapanda-farasi. Hata kama munategemea Misri kupata magari ya vita na waaskari wapanda-farasi, hamuwezi kumurudisha nyuma mutu mumoja wa cheo cha chini sana kati ya watumishi wa bwana wangu. Zaidi ya hayo, munafikiri nimekuja bila amri ya Yawe kwa kuishambulia na kuiangamiza inchi hii? Yawe ndiye aliyeniambia: Uishambulie inchi hii na kuiangamiza!” Kisha Eliakimu mwana wa Hilkia, Sebuna na Yoa wakamujibu yule jemadari: “Tafazali, useme nasi kwa luga ya Kiaramea maana tunaielewa. Usiseme nasi kwa luga ya Kiebrania. Watu wanaokuwa juu ya ukuta wanasikia.” Yule jemadari akawaambia: “Munafikiri kwamba bwana wangu amenituma kutoa ujumbe huu kwa bwana wenu na kwenu tu? Maneno yangu ni vilevile kwa watu wanaoikaa juu ya ukuta! Bado kidogo wao kama vile ninyi watakula mavi yao wenyewe na kunywa mikojo yao wenyewe!” Kisha huyo jemadari akasimama, akalalamika na kusema kwa luga ya Kiebrania: “Musikilize maneno ya mufalme mukubwa, mufalme wa Asuria! Hivi ndivyo mufalme anavyosema: Musikubali Hezekia awadanganye, kwa sababu hataweza kuwaokoa toka katika mikono yangu. Musikubali awashawishi kusudi mumutegemee Yawe, akisema: ‘Yawe atatuokoa na muji huu hautatiwa katika mikono ya mufalme wa Asuria.’ Musimusikilize Hezekia, maana mufalme wa Asuria anasema: ‘Mukuwe na amani nami na kujitoa kwangu. Kisha kila mumoja wenu ataweza kula matunda ya mizabibu yake mwenyewe na matunda ya tini yake mwenyewe na kunywa maji ya kisima chake mwenyewe, mpaka nitakapokuja na kuwapeleka katika inchi kama hii yenu, inchi yenye ngano na divai, inchi yenye mukate na mashamba ya mizabibu, inchi yenye mizeituni na asali, kusudi mupate kuishi, nanyi hamutakufa. Musimusikilize Hezekia anapowadanganya akisema: Yawe atatuokoa. Kuna yoyote kati ya miungu ya mataifa aliyeokoa inchi yake toka katika mikono ya mufalme wa Asuria? Iko wapi ile miungu ya Hamati na Arpadi? Iko wapi ile miungu ya Sefarwaimu, Hena na Iwa? Imeokoa Samaria toka katika mikono yangu? Ni nani kati ya miungu ya inchi hizi aliyeokoa inchi zao toka katika mikono yangu. Yawe ataweza kuukoa Yerusalema?’ ” Lakini watu walinyamaza, wala hawakumujibu neno kama vile walivyoamuriwa na mufalme akisema: “Musimujibu.” Kisha Eliakimu mwana wa Hilkia aliyekuwa musimamizi wa nyumba ya kifalme, Sebuna aliyekuwa katibu, na Yoa mwana wa Asafu mwandishi, wakamwendea Hezekia wakiwa na nguo zenye kupasuliwa, wakamwelezea maneno ya yule jemadari. Mufalme Hezekia aliposikia habari hiyo, alipasua nguo yake, akavaa nguo ya gunia, akaingia katika nyumba ya Yawe. Aliwaamuru Eliakimu, musimamizi wa nyumba ya kifalme, Sebuna mwandishi, na wazee wa makuhani, wamwendee nabii Isaya mwana wa Amozi, wakiwa wamevaa nguo za magunia. Nao wakamwambia Isaya: “Hezekia anasema hivi: ‘Leo ni siku ya huzuni, ya kuazibiwa na ya kuzarauliwa. Sisi tumekuwa kama mwanamuke anayetaka kuzaa mutoto, lakini hana nguvu ya kumuzaa. Labda Yawe, Mungu wako, alisikia maneno ya yule jemadari ambaye ametumwa na bwana wake mufalme wa Asuria, kwa kumutukana Mungu Mwenye Uzima, naye Yawe, Mungu wako atamwazibu kwa ajili ya maneno aliyosikia. Uwaombee watu wanaobaki.’ ” Basi, hao watumishi wa mufalme Hezekia walipokwisha kufika kwa Isaya, aliwaambia: “Mumwambie bwana wenu kwamba Yawe anasema hivi: ‘Usiogope kwa sababu ya maneno uliyoyasikia, ambayo watumishi wa mufalme wa Asuria wameyasema kwa kunitusi. Sikia, nitamufanya mufalme asikie uvumi, halafu atarudi katika inchi yake, na kule nitamufanya auawe kwa upanga.’ ” Kisha yule jemadari aliposikia kwamba mufalme wa Asuria alikuwa ameondoka Lakisi, aliondoka na kumukuta akishambulia muji wa Libuna. Halafu mufalme alipata habari kwamba Tiraka mufalme wa Etiopia anakuja kupigana naye. Akatuma wajumbe kwa Hezekia, akisema: “Mumwambie Hezekia mufalme wa Yuda: ‘Usikubali Mungu wako unayemutegemea akudanganye kwa kukuahidi kwamba Yerusalema hautatekwa na mufalme wa Asuria. Wewe umekwisha kusikia jinsi wafalme wa Asuria walivyotendea inchi nyingine na kuziangamiza kabisa. Unazani wewe utaokoka? Miungu ya mataifa iliokoa Gozani, Harani, na Resefu na Waedeni waliokaa Telasari, mataifa ambayo babu zangu waliyaangamiza? Wako wapi wafalme wa Hamati, Arpadi, Sefarwaimu, Hena na Iwa?’ ” Mufalme Hezekia alipokea barua kutoka kwa wajumbe na kuisoma. Kisha akaenda na kuingia katika nyumba ya Yawe, akaiweka mbele ya Yawe. Halafu akamwomba Yawe akisema: “Ee Yawe, Mungu wa Israeli, unayeikaa katika kiti cha kifalme juu ya makerubi, ni wewe tu unayekuwa Mungu, unayetawala falme zote za ulimwengu. Wewe uliumba dunia na mbingu. Ee Yawe, fumbua macho uone, tega sikio lako uyasikie matusi yote ambayo Saniharibu amepeleka kukutukana wewe Mungu Mwenye Uzima. Ee Yawe, ni kweli kwamba wafalme wa Asuria wameangamiza mataifa na inchi zao. Walitupa miungu yao katika moto kwa sababu haikukuwa miungu ya kweli, lakini sanamu za miti na mawe zilizochongwa na mikono ya watu. Sasa, ee Yawe, Mungu wetu, utuokoe toka katika makucha ya Saniharibu, kusudi falme zote za dunia zijue kwamba ni wewe tu, ee Yawe peke yako, ee Yawe, ambaye ni Mungu.” Kisha Isaya mwana wa Amozi akatuma ujumbe kwa Hezekia, akisema: “Yawe, Mungu wa Israeli anasema hivi: Nimesikia ombi lako kwangu juu ya Saniharibu mufalme wa Asuria. Hili ndilo neno Yawe alilosema juu yake: “Watu wa Sayuni wanakuzarau kabisa, watu wa Yerusalema wanakutikisia kichwa kwa kukuchekelea. Wewe umemutukana nani? Umemutusi nani? Umesubutu kumufokea nani kwa majivuno? Ni Mungu, Mutakatifu wa Israeli! Umewatuma watumishi wako kuchekelea Yawe; wewe umesema: Kwa magari yangu mengi ya vita, nimefika juu kwenye vichwa vya milima, mpaka kwenye vichwa vya milima ya Lebanoni. Nimeangusha mierezi yake mirefu, na misunobari mizurimizuri. Nimevifikia vichwa vyake na ndani ya pori zake kubwa. Nimechimba visima na kunywa maji ya kigeni, nilikausha vijito vya Misri kwa miguu yangu. Haujasikia, ewe Saniharibu, kwamba mimi Yawe nilipanga jambo hili tangu zamani? Ninachotimiza sasa nilikipanga zamani. Nilikuweka uifanye miji yenye kuzungukwa na kuta kuwa lundo la mabomoko. Wakaaji wake wakiwa wameishiwa nguvu, wametishika na kufazaika, wamekuwa kama mimea ya shamba, kama majani changa, kama majani yanayoota juu ya paa, yanayokauka mbele ya kukomaa. Lakini, ninakujua wewe Saniharibu; ninajua wakati unaikaa, wakati unatoka, na wakati unaingia; ninajua vilevile wakati kasirani yako inawaka juu yangu. Kwa vile umefanya mipango juu yangu na nimesikia majivuno yako, nitatia ndoana yangu ndani ya pua yako, na lijamu yangu ndani ya kinywa chako. Nitakurudisha katika njia ileile uliyokuja ndani yake. “Na hiki ndicho kitakuwa kitambulisho kwako Hezekia: Mwaka huu na mwaka unaokuja mutakula kinachoota chenyewe bila kupandwa. Lakini katika mwaka wa tatu mutapanda na kuvuna mavuno; mutapanda mizabibu na kula matunda yake. Wale watakaobaki katika ukoo wa Yuda wataongezeka na kuwa wengi kama vile muti unavyotoa mizizi yake katika udongo na kuzaa matunda juu. Maana kutakuwa watu watakaobaki kule Yerusalema; kule kwenye mulima Sayuni kutakuwa watu wachache watakaobakia. Yawe wa majeshi amekusudia kukamilisha hayo. “Yawe anasema hivi juu ya mufalme wa Asuria: Hataingia katika muji huu, wala kuupiga mushale, wala kuingia akishika ngao, wala hatalundika udongo kandokando yake apate kuubomoa. Atarudi kwa njia ileile aliyokuja nayo wala hataingia katika muji huu. –Ni ujumbe wa Yawe.– Kweli, kwa ajili ya heshima yangu mimi na kwa ajili ya mutumishi wangu Daudi, nitaulinda na kuukoa muji huu.” Basi, malaika wa Yawe aliingia ndani ya kambi ya Waasuria na kuwaua watu elfu mia moja makumi nane na watano. Kesho yake, wakati watu walipoamuka, waliona yale maiti yote. Kisha Saniharibu mufalme wa Asuria akaondoka, akaenda kwake, akakaa Ninawe. Siku moja wakati Saniharibu alipokuwa akiabudu katika nyumba ya Nisiroki mungu wake, wana wake wawili, Adarameleki na Sarezeri walimwua kwa upanga, halafu wakakimbilia katika inchi ya Ararati. Halafu mwana wake Esari-Hadoni akatawala kwa pahali pake. Wakati ule, Hezekia aligonjwa sana karibu kufa. Halafu nabii Isaya, mwana wa Amozi akamwendea, akamwambia: “Yawe amesema hivi: ‘Panga mambo yako sawasawa katika nyumba yako kwa sababu utakufa, hautapona.’ ” Hezekia akageukia upande wa ukuta na kumwomba Yawe, akisema: “Ee Yawe, ninakusihi ukumbuke jinsi nilivyokutumikia kwa uaminifu na kwa moyo wangu wote na kutenda mazuri mbele yako.” Hezekia akalia kwa uchungu sana. Lakini mbele Isaya hajapita kiwanja cha katikati, Yawe akamutolea ujumbe kusema: “Rudi umwambie Hezekia, mukubwa wa watu wa Yawe, na kumwambia: Mimi, Yawe, Mungu wa babu yako Daudi, nimesikia ombi lako na nimeona machozi yako. Nitakuponyesha na nyuma ya siku tatu utaenda katika nyumba ya Yawe. Nitakuongezea miaka kumi na mitano ya kuishi. Nitakuokoa wewe pamoja na muji huu toka katika mikono ya mufalme wa Asuria. Nitaulinda muji huu kwa ajili ya heshima yangu mimi na kwa ajili ya mutumishi wangu Daudi.” Basi Isaya akasema: “Mulete mukate wa tini halafu muutwae na kuuweka kwenye jipu lake, kusudi apate kupona.” Hezekia akamwuliza Isaya: “Ni kitambulisho gani ambacho kitanionyesha kwamba kweli Yawe ataniponyesha na katika siku ya tatu nitaweza kwenda kwa nyumba ya Yawe?” Isaya akamujibu: “Hiki kitakuwa kitambulisho kwako kutoka kwa Yawe, kwamba Yawe atafanya kama alivyoahidi: Unataka kivuli kiende hatua kumi mbele au nyuma?” Hezekia akamujibu: “Ni vyepesi zaidi kivuli kwenda mbele hatua kumi! Basi kirudi nyuma hatua kumi.” Isaya akamwomba Yawe, naye Yawe akafanya kivuli kirudi hatua kumi kwenye ngazi iliyojengwa na Ahazi. Wakati ule, mufalme Berodaki-Baladana mwana wa Baladani mufalme wa Babeli alisikia kwamba Hezekia alikuwa amegonjwa na sasa amepona, alimutumia ujumbe pamoja na zawadi. Basi, Hezekia akawakaribisha na kuwaonyesha mali yake: nyumba yake ya hazina, feza, zahabu, viungo vya kukolezea chakula, mafuta ya bei kali na nyumba ya vifaa vyake vyote vya kiaskari na vitu vyote vilivyokuwa katika akiba zake. Hakukukuwa kitu chochote katika nyumba yake, au inchi yake ambacho hakuwaonyesha. Halafu nabii Isaya akamwendea mufalme Hezekia na kumwuliza: “Watu hawa wamesema nini? Na, wamekujia kutoka wapi?” Naye Hezekia akamujibu: “Wamenifikia kutoka inchi ya mbali.” Halafu akamwuliza: “Wameona nini katika nyumba yako?” Hezekia akamujibu: “Wameona yote yanayokuwa katika nyumba yangu. Hakuna kitu chochote katika akiba zangu ambacho sikuwaonyesha.” Halafu Isaya akamwambia Hezekia: “Sikia neno la Yawe: Siku zinakuja ambapo vyote vinavyokuwa katika nyumba yako na vitu vyote babu zako walivyokusanya mpaka leo, vitapelekwa Babeli. Hakuna kitu chochote kitakachobaki. –Ni Yawe anayesema hivyo.– Tena wamoja kati ya watoto wako wanaume watapelekwa, nao watakuwa matowashi katika nyumba ya mufalme wa Babeli.” Naye Hezekia akamwambia Isaya: “Neno la Yawe ulilosema ni zuri.” Alisema hivyo maana alifikiri: “Kutakuwa amani na salama muda wote wa maisha yangu.” Matendo mengine ya Hezekia, ushujaa wake na maelezo juu ya jinsi alivyojenga kisima na kuchimba mufereji wa kuleta maji katika muji, yameandikwa katika Kitabu cha Mambo ya Siku za Wafalme wa Yuda. Hezekia akakufa, naye mwana wake Manase akatawala kwa pahali pake. Manase alikuwa na umri wa miaka kumi na miwili alipoanza kutawala Yuda, akatawala kutoka Yerusalema kwa muda wa miaka makumi tano na mitano. Alitenda maovu mbele ya Yawe kwa kutenda maovu ya mataifa ambayo yalifukuzwa na Yawe mbele ya watu wa Israeli. Alitengeneza upya nafasi za kuabudia miungu mingine zilizoharibiwa na baba yake Hezekia. Akajenga mazabahu za kuabudia Bali na kutengeneza sanamu ya Ashera, kama vile Ahabu mufalme wa Israeli alivyofanya. Vilevile, Manase aliabudu na kutumikia jeshi la mbingu. Alijenga mazabahu katika nyumba ya Yawe pahali ambapo Yawe alikuwa amesema: “Jina langu litaabudiwa katika Yerusalema.” Katika viwanja viwili vya nyumba ya Yawe, alijenga mazabahu ya kuabudia jeshi la mbingu. Naye alimutoa mwana wake kama sadaka ya kuteketezwa kwa moto. Alipiga ramuli; aliaguza akishirikiana na waaguzi wanaosemezana na mizimu na wachawi. Alitenda maovu mengi mbele ya Yawe, akamukasirikisha. Nayo sanamu ya Ashera aliyotengeneza akaiweka katika nyumba ambayo Yawe alisema juu yake mbele ya Daudi na mwana wake Solomono: “Katika nyumba hii na katika Yerusalema niliouchagua ndipo pahali nitakapoabudiwa milele. Na ikiwa Waisraeli watajali kutenda yote niliyowaamuru na kufuata sheria zote mutumishi wangu Musa alizowapa, basi sitawaacha wafukuzwe kutoka katika inchi hii ambayo niliwapa babu zao.” Lakini hawakusikia, naye Manase aliwasukuma watende zambi zaidi kuliko zile zilizofanywa na mataifa ambayo Yawe aliyaharibu mbele ya Waisraeli. Halafu Yawe akasema kupitia kwa watumishi wake manabii: “Kwa sababu mufalme amefanya mambo ya kuchukiza, mambo mabaya zaidi ya yale yaliyotendwa na Waamori waliomutangulia, akawasukuma watu wa Yuda vilevile watende zambi kwa kutumia sanamu zake, basi, Yawe, Mungu wa Israeli, anasema hivi: Nitaleta juu ya Yerusalema na Yuda hasara ambayo hata yeyote atakayesikia atashituka. Nitauazibu Yerusalema kama vile nilivyofanya Samaria, na mufalme Ahabu na wazao wake. Nitasafisha Yerusalema kama vile wanavyosafisha sahani na kuigeuza kisha kusafishwa. Nitawaacha hao watu wa urizi wangu watakaobaki na kuwaweka katika mikono ya waadui zao, watanyanganywa vitu vyao na kutekwa na waadui zao wote. Nitawatendea hayo yote kwa sababu wameniasi na kunikasirikisha tangia wakati wazee wao walipotoka Misri mpaka leo.” Zaidi ya mambo hayo, Manase aliwaangusha watu wa Yuda katika zambi kwa kutenda maovu mbele ya Yawe. Aliwaua watu wengi wasiokuwa na kosa, damu ikajaa toka upande mumoja mpaka upande mwingine wa Yerusalema. Mambo mengine ya Manase na yote aliyofanya, pamoja na zambi zake zote, yameandikwa katika Kitabu cha Mambo ya Siku za Wafalme wa Yuda. Manase akakufa na kuzikwa katika bustani ya nyumba yake mwenyewe, katika Bustani ya Uza. Naye mwana wake Amoni akatawala kwa pahali pake. Amoni alikuwa na umri wa miaka makumi mbili na mbili alipoanza kutawala, akatawala miaka miwili akiwa kule Yerusalema. Jina la mama yake ni Mesulemeti binti ya Haruzi, wa muji Yotibati. Alitenda maovu mbele ya Yawe, kama vile Manase baba yake alivyofanya. Alifuata njia yote baba yake aliyoiendea na kutumikia sanamu ambazo baba yake alizitumikia na kuziabudu. Alimwacha Yawe, Mungu wa babu zake. Hakushika njia ya Yawe. Kisha watumishi wa Amoni walimwasi na kumwua katika nyumba yake ya kifalme. Lakini watu wa Yuda wakawaua wote waliomwua Amoni. Kisha watu hao wa Yuda wakamuweka mwana wake Yosia kuwa mufalme kwa pahali pake. Matendo mengine yote ya Amoni yameandikwa katika Kitabu cha Mambo ya Siku za Wafalme wa Yuda. Amoni akazikwa katika kaburi katika bustani ya Uza. Yosia mwana wake akatawala kwa pahali pake. Yosia alikuwa na umri wa miaka minane alipoanza kutawala akiwa kule Yerusalema na utawala wake ulidumu kwa miaka makumi tatu na mumoja. Mama yake aliitwa Yedida, binti wa Adaya mukaaji wa muji wa Bozikati. Yosia alitenda kwa usawa mbele ya Yawe. Alifuata mienendo yote ya babu yake Daudi; hakuiacha hata kidogo. Katika mwaka wa kumi na nane wa utawala wake, mufalme alimutuma Safanu mwana wa Azalia, mujukuu wa Mesulamu, mwandishi katika nyumba ya Yawe akisema: “Kwenda kwa Kuhani Mukubwa Hilkia kusudi ahesabu feza zilizoletwa katika nyumba ya Yawe, ambazo walinzi wa mulango walizikusanya kutoka kwa watu; nazo zitolewe kwa wale wanaosimamia kazi ya kutengeneza vizuri nyumba ya Yawe kusudi wapate kuwalipa wafundi wanaofanya kazi ya kutengeneza mabomoko, waseremala, wajengaji na watumishi wengine wenye kujenga, na kununua mbao na mawe yaliyochongwa kwa ajili ya kutengeneza nyumba. Watu wanaosimamia ujenzi wasiombwe kutoa hesabu ya matumizi ya feza watakazopewa, kwa sababu wanazitumia kwa uaminifu.” Kisha Kuhani Mukubwa Hilkia akamwambia Safanu, mwandishi: “Nimekipata kitabu cha Sheria katika nyumba ya Yawe.” Halafu Hilkia akamupatia Safanu kitabu, naye akakisoma. Mwandishi Safanu akamwendea mufalme na kutoa habari, akisema: “Watumishi wako wametoa feza zilizopatikana katika nyumba, halafu wakazipeleka kwa wafundi wanaosimamia kazi ya kutengeneza nyumba ya Yawe.” Kisha Safanu, mwandishi akamwambia mufalme: “Kuhani Hilkia amenipa kitabu.” Naye Safanu akakisoma mbele ya mufalme. Mufalme aliposikia maneno ya Kitabu cha Sheria, akapasua nguo zake. Akaamuru kuhani Hilkia, Ahikamu mwana wa Safanu na Akibori mwana wa Mikaya pamoja na mwandishi Safanu na Asaya mutumishi wa mufalme, akisema: “Mwende muombe shauri kutoka kwa Yawe kwa ajili yangu, na kwa watu wa Yuda wote juu ya maneno ya kitabu hiki kilichopatikana kwa sababu kasirani ya Yawe imewaka juu yetu, maana babu zetu hawakutii maneno ya kitabu hiki na kutimiza yote yaliyoandikwa juu yetu.” Kwa hiyo kuhani Hilkia, Ahikamu, Akibori, Safanu na Asahiya, wote walikwenda kuomba shauri kwa mwanamuke mumoja nabii jina lake Hulda aliyekuwa muke wa Salumu mwana wa Tikwa, mujukuu wa Harihasi, mutunza nguo za hekalu. Wakati ule, Hulda alikuwa anaishi katika mutaa wa pili wa Yerusalema, nao wakazungumuza naye. Basi akawaambia: “Hivi ndivyo Yawe, Mungu wa Israeli, anavyosema: Mumwambie yule aliyewatuma kwangu, Yawe anasema hivi: Nitaleta uovu juu ya pahali hapa na juu ya wakaaji wake kama vile inavyokuwa katika kitabu kilichosomwa na mufalme wa Yuda. Kwa sababu wameniacha na kufukizia miungu mingine ubani kusudi watu wanikasirikishe kwa kazi zote za mikono yao, basi, kasirani yangu juu ya Yerusalema itawaka na haitaweza kutulizwa. Lakini juu ya mufalme wa Yuda aliyewatuma kuomba shauri la Yawe, mumwambie kwamba, hivi ndivyo Yawe, Mungu wa Israeli anavyosema juu ya maneno uliyoyasikia. Wakati uliposikia niliyosema juu ya pahali hapa na juu ya wakaaji wake, kwamba watakuwa ukiwa na kulaaniwa, ulijuta na kunyenyekea mbele yangu, hata ukapasua nguo yako na kulia mbele yangu. Basi, nami vilevile nimekusikia. Kwa hiyo, nitakukusanya pamoja na babu zako nawe utazikwa katika kaburi kwa amani, macho yako hayataona uovu nitakaoleta juu ya pahali hapa.” Basi wajumbe wakamuletea mufalme Yosia habari hii. Kisha mufalme akatuma wajumbe, nao wakamukusanyia viongozi wote wa Yuda na wa Yerusalema. Naye mufalme akaenda katika nyumba ya Yawe pamoja na watu wote wa Yuda na wakaaji wote wa Yerusalema, na makuhani pamoja na manabii, watu wote, wadogo kwa wakubwa. Basi, akawasomea maneno ya kitabu cha agano kilichopatikana katika nyumba ya Yawe. Halafu mufalme akasimama karibu na nguzo na kufanya agano mbele ya Yawe, kumufuata Yawe, kushika amri zake, maagizo na masharti yake kwa moyo wake wote na kwa roho yake yote, kutenda maneno yote ya agano yaliyoandikwa katika kitabu hicho; nao watu wote wakaungana katika kufanya agano. Kisha Yosia akaamuru Kuhani Mukubwa Hilkia na makuhani wasaidizi wake na walinzi wa mulango watoe katika hekalu la Yawe vitu vilivyotengenezwa kwa ajili ya Bali, Ashera na kwa ajili ya jeshi la mbingu. Aliviteketeza inje ya Yerusalema katika bonde la Kidroni na kupeleka majivu yake kule Beteli. Kisha akawaondoa makuhani wote waliobarikiwa na wafalme wa Yuda kwa kufukiza ubani katika pahali pa kuabudia katika miji ya Yuda na kunzunguka Yerusalema, vilevile wale waliofukiza ubani kwa Bali, jua, mwezi, nyota na jeshi la mbingu katika nyumba ya Yawe. Naye aliondoa sanamu ya Ashera kutoka katika nyumba ya Yawe, inje ya Yerusalema, akaipeleka mpaka kwenye kijito cha Kidroni. Kule akaiteketeza na kuisaga mpaka ikakuwa mavumbi, nayo mavumbi yake akayatawanya juu ya makaburi ya watu. Alibomoa nyumba za makahaba zilizokuwa katika nyumba ya Yawe, pahali wanawake walifuma mapazia ya Ashera. Akakusanya makuhani wote kutoka miji ya Yuda na aliharibu pahali pa kuabudia makuhani walipofukiza ubani, kutoka Geba mpaka Beri-Seba. Akabomoa pahali pa kuabudia palipokuwa upande wa kushoto wa mulango wa muji kwenye milango iliyokuwa kwenye njia ya kuingilia kwenye mulango wa Yoshua mutawala wa muji. Makuhani hao hawakufikia mazabahu ya Yawe katika Yerusalema, lakini walikula mikate isiyotiwa chachu waliyopewa na makuhani wenzao. Mufalme Yosia aliharibu pahali pa kuabudia miungu ya uongo palipoitwa Tofeti katika bonde la wana wa Hinomu, kusudi mutu yeyote asimuteketeze mwana wake au binti yake kama sadaka kwa Moleki. Vilevile aliondoa farasi waliotengwa na wafalme wa Yuda kwa ajili ya kuabudu jua kwenye njia ya kuingia katika nyumba ya Yawe, karibu na chumba cha Natani-Meleki, kilichokuwa inje ya muji; naye alichoma kwa moto magari ya jua. Mazabahu ambayo wafalme wa Yuda walijenga juu ya paa kwenye chumba cha juu cha Ahazi, pamoja na mazabahu ambayo Manase alijenga katika viwanja viwili vya nyumba ya Yawe, aliyabomoa na kuyapondaponda, kisha alitupa mavumbi yake katika kijito cha Kidroni. Vilevile aliharibu pahali pa kuabudia palipokuwa upande wa mashariki ya Yerusalema na kuelekea upande wa mulima wa uharibifu, pahali mufalme wa Israeli alipopajenga kwa ajili ya Astaroti chukizo la Wasidoni, Kemosi chukizo la Moabu na vilevile kwa ajili ya Milkomu chukizo la Waamoni. Alivunja nguzo vipandevipande; vilevile alikatakata sanamu za Ashera, na pahali zilipokuwa zinasimama akapajaza mifupa ya watu. Zaidi ya hayo aliharibu kule Beteli pahali pa kuabudia palipojengwa na mufalme Yeroboamu mwana wa Nebati ambaye aliwasukuma watu wa Israeli watende zambi. Aliharibu mazabahu hayo na kuvunja mawe yake vipandevipande, na kisha akaviponda mpaka vikakuwa mavumbi. Vilevile akachoma sanamu ya Ashera. Kisha Yosia alipogeuka akaona makaburi juu ya kilima. Aliagiza mifupa ifukuliwe kutoka makaburi na kuichoma juu ya mazabahu. Basi akachafua mazabahu sawasawa na neno la Yawe ambalo mutu wa Mungu alilitangaza, nabii ambaye alitabiri matukio haya. Halafu mufalme akauliza: “Munara ninaouona kule ni wa nini?” Nao watu wa muji wakamujibu: “Ni kaburi la mutu wa Mungu ambaye alikuja kutoka Yuda na kutabiri mambo ambayo umeyafanya juu ya mazabahu pale Beteli.” Naye akaagiza: “Umwache pale, mutu yeyote asiondoe mifupa yake.” Kwa hiyo waliiacha mifupa yake, pamoja na mifupa ya nabii aliyetoka Samaria. Katika kila muji wa Samaria mufalme Yosia aliharibu pahali pa kuabudia miungu ya uongo palipojengwa na wafalme wa Israeli, kwa kumutukana Yawe. Mazabahu hayo yote aliyaharibu kama vile alivyofanya kule Beteli. Aliwaua makuhani wote wa miungu ya uongo juu ya mazabahu ambapo walitumikia na kuchoma mifupa yao juu ya mazabahu hayo. Kisha akarudi Yerusalema. Kisha mufalme akawaamuru watu wote, akisema: “Mumufanyie Yawe, Mungu wenu, Pasaka, kama ilivyoandikwa katika kitabu hiki cha agano.” Hakuna Pasaka iliyosherehekewa kama hii tangu wakati wa waamuzi waliowaongoza Waisraeli wala wakati wa wafalme wa Israeli au wa Yuda. Lakini, katika mwaka wa kumi na nane wa utawala wa Yosia, Pasaka ilisherehekewa kwa Yawe katika Yerusalema. Tena, kusudi mufalme Yosia atimize sheria zote zilizoandikwa katika kitabu Kuhani Mukubwa Hilkia alichokipata katika nyumba ya Yawe, aliondoa wachawi, watabiri, miungu, sanamu za miungu pamoja na vyombo vingine vilivyotumika kwa kuabudu miungu ya uongo kutoka inchi ya Yuda na kutoka Yerusalema. Mbele ya Yosia au nyuma yake hakuna mufalme yeyote aliyekuwa kama yeye, ambaye alimutumikia Yawe kwa moyo wake wote, kwa nguvu zake zote na kwa roho yake yote kulingana na Sheria ya Musa. Hata hivyo, Yawe hakuacha ukali wa kasirani yake nyingi, kwa sababu hasira yake iliwaka juu ya Yuda kwa ajili ya vitendo vya kukasirikisha, ambavyo Manase alifanya juu yake. Naye Yawe akasema: “Nitawafukuza watu wa Yuda kutoka mbele yangu kama vile nilivyofanya kwa watu wa Israeli. Nitaukataa muji wa Yerusalema ambao niliuchagua niliposema: ‘Jina langu litakuwa mule.’ ” Mambo mengine ya Yosia na yote aliyofanya yameandikwa katika Kitabu cha Mambo ya Siku za Wafalme wa Yuda. Wakati wa kutawala kwake, Neko mufalme wa Misri alikwenda mpaka kwenye muto Furati kwa kukutana na mufalme wa Asuria. Naye mufalme Yosia akaondoka kwa kupigana naye; lakini Neko mufalme wa Misri alipomwona akamwua kule Megido. Wakubwa wake wakaibeba maiti yake katika gari na kuirudisha Yerusalema walikomuzika katika kaburi lake mwenyewe. Kisha watu wa Yuda wakamuchukua Yoahazi mwana wa Yosia, wakamupakaa mafuta na kumuweka kuwa mufalme kwa pahali pa baba yake. Yoahazi alikuwa na umri wa miaka makumi mbili na tatu alipoanza kutawala, akatawala kwa miezi mitatu akiwa kule Yerusalema. Mama yake aliitwa Hamutali, binti ya Yeremia wa muji wa Libuna. Yoahazi alitenda maovu mbele ya Yawe kama yote babu zake waliyofanya. Kusudi asiendelee kutawala akiwa kule Yerusalema, Neko mufalme wa Misri alimufunga kule Ribla katika inchi ya Hamati, akawalipisha watu wa Yuda kodi ya kilo elfu tatu na mia ine za feza na kilo makumi tatu na ine za zahabu. Neko mufalme wa Misri akamuweka Eliakimu mwana wa mufalme Yosia kwa pahali pa baba yake Yosia, akabadilisha jina lake kuwa Yoyakimu. Lakini alimupeleka Yoahazi mbali. Naye akafika Misri na kukufia kule. Mufalme Yoyakimu akamupa Mufalme wa Misri feza na zahabu, lakini akailipisha inchi kodi kusudi aweze kutimiza mapenzi ya Mufalme wa Misri ya kupewa feza. Akawalipisha wanainchi feza na zahabu. Kila mumoja alitoa kufuatana na kiasi mufalme alichoamuru, naye akamupa Neko mufalme wa Misri. Yoyakimu alikuwa na umri wa miaka makumi mbili na tano alipoanza kutawala, na akatawala akiwa Yerusalema kwa muda wa miaka kumi na mumoja. Jina la mama yake lilikuwa Zebuda binti wa Pedaya wa muji wa Ruma. Yoyakimu alitenda maovu mbele ya Yawe, kama vile yote babu zake waliyofanya. Nebukadneza mufalme wa Babeli akaishambulia inchi ya Yuda. Yoyakimu akamutumikia kwa miaka mitatu halafu akaacha kumutii, akamwasi. Basi, Yawe akamupelekea makundi ya Wababeli, Waaramu, Wamoabu na Waamoni washambulie inchi ya Yuda na kuiharibu, kulingana na neno la Yawe alilolisema kwa njia ya watumishi wake manabii. Hakika mambo haya yakaitokea inchi ya Yuda kwa amri ya Yawe, kwa kuwahamisha kutoka mbele yake, kwa sababu ya zambi za mufalme Manase na yote aliyoyatenda, na kwa sababu ya damu isiyokuwa na kosa aliyoimwanga. Yawe hakumusamehe makosa hayo. Basi mambo mengine ya Yoyakimu na yote aliyofanya yameandikwa katika Kitabu cha Mambo ya Siku za Wafalme wa Yuda. Yoyakimu akakufa, na mwana wake Yoyakini akatawala kwa pahali pake. Mufalme wa Misri hakutoka tena katika inchi yake, kwa sababu mufalme wa Babeli alinyanganya inchi yote iliyokuwa mali ya Misri pale zamani, tangia kwenye kijito cha Misri mpaka kwenye muto Furati. Yoyakini alikuwa na umri wa miaka kumi na minane alipoanza kutawala. Alitawala akiwa Yerusalema kwa muda wa miezi mitatu. Mama yake aliitwa Nehusta, binti ya Elnatani, mukaaji wa Yerusalema. Alitenda maovu mbele ya Yawe kama vile baba yake alivyofanya. Wakati ule waaskari wa Nebukadneza mufalme wa Babeli wakashambulia Yerusalema na kuuzunguka. Wakati waaskari walipokuwa wanauzunguka muji, Nebukadneza mwenyewe alifika Yerusalema, na Yoyakini mufalme wa Yuda alijitoa kwa mufalme wa Babeli, yeye mwenyewe pamoja na mama yake, watumishi wake, wakubwa na majemadari wake. Mufalme wa Babeli aliwapeleka kama wafungwa katika mwaka wa nane wa kutawala kwake. Tena kama vile Yawe alivyosema, Nebukadneza alitwaa mali yote iliyokuwa ndani ya nyumba ya Yawe, na ndani ya nyumba ya kifalme. Akakatakata vyombo vyote vya zahabu ambavyo Solomono mufalme wa Israeli alitengeneza. Vyombo hivyo vilikuwa ndani ya hekalu la Yawe. Alitwaa watu wote wa Yerusalemu: wakubwa wote, watu wote waliokuwa mashujaa, wafungwa elfu kumi, na wafundi wote na wafuaji wa vyuma. Hakuna aliyebaki isipokuwa wale waliokuwa wamasikini kabisa katika inchi. Alimupeleka Yoyakini mpaka Babeli pamoja na mama ya mufalme, wake za mufalme, wakubwa wa waaskari wake, na wakubwa wa inchi wote. Hao aliwatoa Yerusalema. Akawapeleka katika uhamisho kule Babeli. Nebukadneza alipeleka watu mashujaa wa Yuda, jumla yao watu elfu saba pamoja na wafundi hodari na wafuaji wa vyuma elfu moja, wote hawa wakiwa watu wenye nguvu na wa kuweza kupigana katika vita. Nebukadneza akamuweka Matania, baba mudogo ya Yoyakini, kuwa mufalme kwa pahali pake, akalibadilisha jina lake kuwa Zedekia. Zedekia alikuwa na umri wa miaka makumi mbili na mumoja alipoanza kutawala, alitawala kwa muda wa miaka kumi na mumoja akiwa kule Yerusalema. Mama yake aliitwa Hamutali binti wa Yeremia, mukaaji wa muji wa Libuna. Alitenda maovu mbele ya Yawe. Alifuata yote Yoyakimu aliyofanya. Yawe aliwakasirikia sana watu wa Yerusalema na Yuda, hata akawafukuza mbali naye. Zedekia alimwasi mufalme wa Babeli. Katika siku ya kumi ya mwezi wa kumi, mwaka wa tisa wa utawala wa Zedekia, Nebukadneza mufalme wa Babeli akafika na waaskari wake kwa kushambulia Yerusalema. Akapiga kambi mbele ya muji ule na kujenga ngazi kuuzunguka. Muji uliendelea kuzungukwa mpaka mwaka wa kumi na moja wa utawala wa Zedekia. Katika siku ya tisa ya mwezi wa ine njaa ilikuwa kali sana katika muji hata hakukuwa chakula chochote kwa ajili ya wakaaji wake. Basi, sehemu ya ukuta wa muji ukabomolewa, naye mufalme pamoja na waaskari wote wakakimbia wakati wa usiku wakipitia katika bustani ya mufalme kwenye mulango katikati ya kuta mbili, wakaenda upande wa Araba, ingawa Wababeli walikuwa wameuzunguka muji. Lakini waaskari wa Babeli wakamufuata mufalme na kumuteka kwenye bonde za Yeriko, nao waaskari wake wote wakamwacha, wakatawanyika. Basi, Wababeli wakamuteka mufalme, wakamupeleka kwa mufalme wao kule Ribla, naye akamuhukumu. Halafu wakawaua wana wa Zedekia mbele yake, kisha wakamwongoa macho yake. Kwa mwisho wakamufunga kwa minyororo, wakamupeleka Babeli. Katika siku ya saba ya mwezi wa tano wa mwaka wa kumi na tisa wa utawala wa Nebukadneza mufalme wa Babeli, Nebuzaradani mukubwa wa waaskari walinzi wa mufalme, akaingia Yerusalema. Akaichoma kwa moto nyumba ya Yawe, nyumba ya kifalme na nyumba zote za Yerusalema; kila nyumba kubwa akaichoma kwa moto. Nao waaskari wote wa Babeli waliokuwa pamoja na mukubwa wa waaskari na walinzi wa mufalme walizibomoa kuta zilizouzunguka Yerusalema. Nebuzaradani, mukubwa wa waaskari wa mufalme, akawapeleka katika uhamisho watu waliokuwa wamebakia katika muji na wale wote waliokuwa wamejitoa wenyewe kwa mufalme wa Babeli pamoja na watu wengine wote. Lakini aliacha wamoja wa watu waliokuwa wamasikini kabisa katika inchi. Aliwaacha watunze mizabibu na kulima mashamba. Wababeli walivunja vipandevipande nguzo za shaba ambazo zilikuwa katika nyumba ya Yawe, pamoja na viikalio vya birika kubwa la shaba nyeusi lililokuwa mule katika nyumba ya Yawe, wakapeleka shaba nyeusi mpaka Babeli. Vilevile walipeleka vyungu, majembe, makasi na miiko iliyotumiwa kwa kuchoma ubani na vyombo vingine vyote vya shaba nyeusi vilivyotumiwa katika kazi ya hekalu, wakapeleka vyetezo na mabakuli. Mukubwa wa waaskari walinzi wa mufalme akapeleka mbali kila chombo cha zahabu na kila chombo cha feza. Shaba yote nyeusi Solomono aliyotumia kwa kutengeneza zile nguzo mbili, birika lile kubwa na viikalio kwa ajili ya nyumba ya Yawe haikuweza kupimwa kwa uzito. Kila nguzo ilikuwa na urefu wa metre nane, na juu yake kulikuwa kichwa cha shaba nyeusi. Urefu wa kila kichwa ulikuwa metre moja na sentimetre makumi mbili na tano. Kila kichwa kilizungushiwa mapambo ya makomamanga, yote ya shaba nyeusi. Kisha Nebuzaradani mukubwa wa waaskari walinzi wa mufalme akamupeleka Seraya, Kuhani Mukubwa, kuwa mufungwa pamoja na Zefania, kuhani wa pili, na wakubwa wa walinda milango watatu. Akamupeleka jemadari mumoja kule katika muji ambaye alikuwa akiwaongoza waaskari katika vita, pamoja na watu watano wenye heshima wa mufalme ambao aliwakuta kule. Vilevile, akamupeleka katibu wa jemadari wa waaskari ambaye alichunga habari za kuandika waaskari wapya pamoja na watu makumi sita wenye heshima ambao aliwakuta Yerusalema. Nebuzaradani mukubwa wa waaskari walinzi akawatwaa watu hao, akawapeleka kwa mufalme wa Babeli kule Ribla. Mufalme Nebukadneza wa Babeli akawapiga na kuwaua watu hao kule Ribla katika inchi ya Hamati. Hivyo watu wa Yuda wakapelekwa kuwa watumwa inje ya inchi yao. Mufalme Nebukadneza wa Babeli akamuchagua Gedalia mwana wa Ahikamu, mujukuu wa Safanu, kuwa mutawala wa watu wote wa Yuda ambao hawakupelekwa Babeli. Kisha wakubwa wote wa waaskari pamoja na watu wao waliposikia kwamba mufalme wa Babeli alimuchagua Gedalia kuwa mutawala, wakamwendea Gedalia kule Mispa. Watu hao walikuwa ni: Isimaeli mwana wa Netania, Yohana mwana wa Karea, Seraya mwana wa Taumeti wa muji wa Netofati, na Yazania mwana wa Mumakati. Naye Gedalia aliapa mbele yao na watu wao, akasema: “Musiogope kwa sababu ya wakubwa wa Wababeli. Mukae katika inchi mumutumikie mufalme wa Babeli na mambo yote yatawaendekea vema.” Katika mwezi wa saba, Isimaeli mwana wa Netania, mujukuu wa Elisama, aliyekuwa wa ukoo wa kifalme, akafika kwa Gedalia pamoja na watu kumi, akamushambulia Gedalia, akamwua. Vilevile, akawaua Wayuda na Wababeli waliokuwa naye. Halafu, Waisraeli wote, wadogo na wakubwa pamoja na wakubwa wa waaskari wakaondoka, wakaenda Misri, kwa sababu waliwaogopa Wababeli. Katika mwaka wa makumi tatu na mbili, Ewili-Merodaki mufalme wa Babeli alianza kutawala. Mwaka uleule akamusamehe Yoyakini mufalme wa Yuda, akamufungua. Hayo yalitokea katika siku ya makumi mbili na saba ya mwezi wa kumi na mbili wa mwaka wa makumi tatu na saba tangu Yoyakini alipopelekwa katika uhamisho. Aliongea naye vizuri na kumupa nafasi ya heshima kuliko wafalme wengine waliokuwa pamoja naye kule Babeli. Basi, Yoyakini akabadilisha nguo zake za mufungwa. Kila siku alikuwa anapata chakula chake kwa mufalme siku zote za maisha yake. Alipatiwa na mufalme posho yake siku kwa siku, kwa muda wa maisha yake yote kufuatana na mahitaji yake. Wana wa Yafeti walikuwa: Gomeri, Magogi, Madayi, Yavani, Tubali, Meseki na Tirasi. Wana wa Gomeri walikuwa: Askenazi, Rifati na Togarma. Wana wa Yavani walikuwa: Elisha, Tarsisi, Kitimu na Roda. Wazao wa Misri ni: Waludi, Waanami, Walehabi, Wanafutuhi, Wapatirusi Wakafutori na Wakasiluhi (hao ndio asili ya Wafilistini). Wana wa Kanana walikuwa: Sidoni, muzaliwa wake wa kwanza, na Heti. Kanana vilevile ndiye babu ya Wayebusi, Waamori, Wagirgasi, Wahivi, Waarki, Wasini, Waarwadi, Wasemari na Wahamati. Wana wa Semu walikuwa: Elamu, Asuri, Arpakisadi, Ludi, Aramu, Usi, Huli, Geteri na Meseki. Arpakisadi alikuwa baba ya Sela. Sela alikuwa baba ya Eberi. Eberi alikuwa na wana wawili: mumoja wao aliitwa Pelegi, ni kusema “Matengano”, kwa maana wakati wake watu walikuwa wametawanyika katika dunia, na ndugu yake aliitwa Yokitani. Wana wa Yokitani walikuwa: Almodadi, Selefu, Hazarmaweti, Yera, Hadoramu, Uzali, Dikla, Ebali, Abimaeli, Seba, Ofiri, Havila na Yobabu. Hawa wote ni wana wa Yokitani. Abrahamu alikuwa na wana wawili: Isaka na Isimaeli. Isimaeli alikuwa baba ya: Nebayoti, ndiye muzaliwa wake wa kwanza, Kedari, Abudeli, Mibusami, Misima, Duma, Masa, Hadadi, Tema, Yeturi, Nafisi na Kedema. Hao ndio wana wa Isimaeli. Abrahamu alikuwa na habara aliyeitwa Ketura. Ketura alimuzalia Abrahamu: Simurani, Yokisanu, Medani, Midiani, Isibaki na Sua. Wana wa Yokisanu walikuwa: Seba na Dedani. Wana wa Midiani walikuwa: Efa, Eferi, Hanoki, Abida na Eldaa. Wote hawa walikuwa wana wa Ketura. Isaka, mwana wa Abrahamu, alikuwa na wana wawili: Esau na Israeli. Wana wa Esau walikuwa: Elifasi, Rueli, Yeusi, Yalamu na Kora. Wana wa Elifasi walikuwa: Temani, Omari, Zefi, Gatamu, Kenasi, Timuna na Amaleki. Wana wa Rueli walikuwa: Nahati, Zera, Sama na Miza. Wana wa Seiri walikuwa: Lotani, Zobali, Sibeoni, Ana, Disoni, Ezeri na Disani. Wana wa Lotani walikuwa: Hori na Homamu. Lotani alikuwa na dada yake aliyeitwa Timuna. Wana wa Sobali walikuwa: Aliani, Manahati, Ebali, Sefi na Onamu. Wana wa Sibeoni walikuwa: Aya na Ana. Mwana wa Ana alikuwa: Disoni. Wana wa Disoni walikuwa: Hamurani, Esibani, Itirani na Kerani. Wana wa Ezeri walikuwa: Bilihani, Zawani na Yakani. Wana wa Disoni walikuwa: Usi na Arani. Wana wa Israeli walikuwa: Rubeni, Simeoni, Lawi, Yuda, Isakari, Zebuluni, Dani, Yosefu, Benjamina, Nafutali, Gadi na Aseri. Wana wa Peresi walikuwa: Hesironi na Hamuli. Wana wa Zera walikuwa watano: Simuri, Etani, Hemanu, Kalkoli na Dara. Mwana wa Karmi alikuwa: Akana, ni kusema “Taabu”. Huyu aliwaletea Waisraeli taabu kwa sababu alijiwekea vitu vilivyolaaniwa. Mwana wa Etani alikuwa: Azaria. Wana wa Hesironi walikuwa: Yerameli, Ramu na Kelubai. Yese alizaa: Eliabu, muzaliwa wake wa kwanza, wa pili Abinadabu, wa tatu Simea, wa ine Netaneli, wa tano Radai, wa sita Osemu na wa saba Daudi. Wadada zao walikuwa Zeruya na Abigaili. Wana wa Zeruya walikuwa watatu: Abisai, Yoabu na Asaheli. Abigaili alikuwa baba ya Amasa ambaye baba yake alikuwa Yeteri, Mwisimaeli. Kalebu mwana wa Hesironi, kutoka kwa bibi zake wawili Azuba na Yerioti, alizaa: Yeseri, Sobabu na Ardoni. Azuba alipokufa, Kalebu akaoa Efurata aliyemuzalia Huri. Huri alikuwa baba ya Uri, naye Uri alizaa Besaleli. Hesironi alipokuwa na umri wa miaka makumi sita, akaoa binti ya Makiri, dada ya Gileadi. Huyu akamuzalia mwana jina lake Segubu. Segubu alizaa Yairi ambaye alitawala miji mikubwa makumi mbili na mitatu katika inchi ya Gileadi. Lakini falme za Gesuri na Aramu ziliwashambulia na kuwanyanganya miji ya Yairi, Kenati pamoja na vijiji vyake, jumla ya miji ilikuwa makumi sita. Hao wote walikuwa wazao wa Makiri, baba ya Gileadi. Nyuma ya kufa kwa Hesironi, Kalebu akaoa Efurata, mujane wa baba yake Hesironi. Efurata akamuzalia Kalebu mwana jina lake Asuri, aliyekuwa mwanzilishi wa muji wa Tekoa. Yerameli, muzaliwa wa kwanza wa Hesironi, alikuwa na wana watano: Ramu, muzaliwa wake wa kwanza, Buna, Oreni, Osemu na Ahiya. Yerameli alikuwa na muke mwingine jina lake Atara. Yeye akamuzalia Yerameli mwana, jina lake Onamu. Wana wa Ramu, muzaliwa wa kwanza wa Yerameli, walikuwa: Masi, Yamini na Ekeri. Wana wa Onamu walikuwa: Samayi na Yada. Nao wana wa Samayi walikuwa Nadabu na Abisuri. Abisuri akaoa muke, jina lake Abihaili, naye akamuzalia wana wawili: Abani na Molidi. Wana wa Nadabu walikuwa: Seledi na Apaimu. Seledi akakufa bila watoto. Mwana wa Apaimu alikuwa: Isi. Mwana wa Isi: Sesani. Mwana wa Sesani: Alai. Wana wa wawili wa Yada, ndugu ya Samai: Yeteri na Yonatani. Yeteri alikufa bila watoto. Yonatani alikuwa na wana wawili: Peleti na Zaza. Wote hawa ni wazao wa Yerameli. Sesani hakukuwa na watoto wa kiume; alikuwa na wabinti tu. Hata hivyo, alikuwa na mutumwa wa Mumisri, jina lake Yara. Hivyo, Sesani akamupa Yara mutumwa wake, mumoja kati ya wabinti zake kuwa muke wake, naye akamuzalia mwana jina lake Atai. Muzaliwa wa kwanza wa Kalebu, ndugu ya Yerameli, aliitwa Mesa. Mesa alikuwa baba ya: Zifu, Zifu baba ya Maresa, Maresa alizaa Hebroni. Wana wa Hebroni walikuwa: Kora, Tapua, Rekemu na Sema. Sema alizaa Rahamu na babu ya Rekemu. Rekemu alizaa Samai. Samai alizaa Maoni, Maoni alizaa Beti-Suri. Kalebu alikuwa na habara, jina lake Efa. Huyu akamuzalia wana wengine watatu: Harani, Moza na Gazezi. Harani alizaa Gazezi. Yadai alikuwa na wana sita: Regemu, Yotamu, Gesani, Peleti, Efa na Safu. Kalebu alikuwa na wazao wengine vilevile toka kwa muke wake Efurata. Wana wa Huri, muzaliwa wake wa kwanza, walikuwa: Sobali, mwanzilishi wa muji wa Kiriati-Yearimu; Salma, mwanzilishi wa muji wa Betelehemu, na Harefu, mwanzilishi wa muji wa Beti-Gaderi. Sobali, mwanzilishi wa muji wa Kiriati-Yearimu, alikuwa vilevile babu ya: watu wa Haroe, na nusu ya wakaji wa muji wa Menuhoti, pamoja na ukoo hizi zilizoishi Kiriati-Yearimu: Waitiri, Waputi, Wasumati na Wamisira. (Wazorati na Waestaoli walitoka katika watu wale). Salma, mwanzilishi wa muji wa Betelehemu alikuwa babu ya: Wanetofati, Waataroti-Beti-Yoabu na nusu ya Wamenahati ni kusema Wazori. Watu wa jamaa hizi waliishi katika muji wa Yabesi: Watirati, Wasimeati na Wasukati. Wao ndio Wakeni waliotoka katika uzao wa Hamati, aliyekuwa babu ya waliokuwa wa ukoo wa Warekabu. Wote sita, walizaliwa Hebroni ambako Daudi alitawala kwa muda wa miaka saba na nusu. Kule Yerusalema, alitawala kwa muda wa miaka makumi tatu na mitatu. Hawa ndio wana wa mufalme Daudi waliozaliwa alipokuwa Yerusalema: Muke wake Bati-Seba, binti ya Amieli, akamuzalia wana wane: Simea, Sobabu, Natani na Solomono. Na zaidi ya hao alikuwa na wana wengine tisa: Ibuhari, Elisua, Elifeleti, Noga, Nefegi, Yafia, Elisama, Eliada na Elifeleti. Hao wote walikuwa wana wa Daudi, zaidi ya wale kuna wengine aliozaliwa na wahabara yake. Daudi alikuwa na binti vilevile, aliyeitwa Tamari. Wana wa Yosia walikuwa: Yohana, muzaliwa wake wa kwanza; wa pili Yoyakimu, wa tatu Zedekia na wa ine Salumu. Wana wa Yoyakimu walikuwa: Yekonia na Zedekia. Wana wa Yekonia, aliyepelekwa kuwa mufungwa na Wababeli, walikuwa: Saltieli, Malkiramu, Pedaya, Senazari, Yekamia, Hosama na Nedabia. Wana wa Pedaya walikuwa: Zerubabeli na Simei. Wana wa Zerubabeli walikuwa: Mesulamu na Hanania. Alikuwa na binti mumoja, jina lake Selomiti. Zerubabeli vilevile alikuwa na wana wengine watano: Hasuba, Oheli, Berekia, Hasadia na Yusabu-Hesedi. Wana wa Hanania walikuwa: Pelatia na Yesaya. Mwana wa Yesaya: Refaya. Mwana wake: Arnani. Mwana wake: Obadia. Mwana wake: Sekania. Mwana wa Sekania: Semaya. Wana wa Semaya walikuwa sita: Hatusi, Igali, Baria, Nearia na Safati. Nearia alikuwa na wana watatu: Eliyoenai, Hezekia na Azirikamu. Eliyoenai alikuwa na wana saba: Hodavia, Eliasibu, Pelaya, Akubu, Yohana, Dalaya na Anani. Wana wa Yuda walikuwa: Peresi, Hesironi, Karmi, Huri na Sobali. Raya mwana wa Sobali, alizaa Yahati, aliyekuwa baba ya Ahumai na Lahadi, hizo ndizo jamaa za Wazorati. Wana wa Etamu walikuwa: Yezereheli, Isima na Idubasi. Walikuwa na dada mumoja aliyeitwa Hasilelponi. Penueli alizaa Gedori na Ezeri, na Ezeri alizaa Husa. Hawa ndio wazao wa Huri muzaliwa wa kwanza wa Efurata, watu wa muji wa Betelehemu. Asuri, mwanzilishi wa muji wa Tekoa, alikuwa na wake wawili: Hela na Nara. Nara akamuzalia wana wane: Ahuzamu, Heferi, Temeni na Ahastari. Hela akamuzalia wana watatu: Zereti, Izihari na Etinani. Hakosi alizaa Anubu na Zobeba, na ndiye aliyekuwa baba wa jamaa za wazao wa Aharheli mwana wa Harumu. Kulikuwa mutu mumoja jina lake Yabesi, aliyeheshimiwa kuliko wandugu zake wote. Mama yake alimupa jina la Yebesi kwa sababu alizaa kwa maumivu. Lakini Yebesi alimwomba Mungu wa Israeli akisema: “Ee Mungu, ninakusihi unibariki na kupanua mipaka yangu. Mukono wako ukuwe pamoja nami na unilinde kutokana na jambo lolote ovu, na mateso yasinipate.” Naye Mungu akamupa yale aliyoomba. Kelubi, ndugu ya Sua, alizaa Mehiri. Mehiri alizaa Estoni. Estoni alizaa: Beti-Rafa, Pasea na Tehina. Tehina alikuwa mwanzilishi wa muji wa Iri-Nahasi. Wazao wa watu hawa waliishi Reka. Wana wa Kenasi walikuwa: Otieli na Seraya. Wana wa Otieli walikuwa: Hatati na Meonotai. Meonotai alizaa Ofura. Seraya alizaa Yoabu, mwanzilishi wa Bonde la Wafundi, lililopewa jina hilo kwa sababu wote waliokuwa mule walikuwa wafundi kabisa. Wana wa Kalebu, mwana wa Yefune, walikuwa: Iru, Ela na Nama. Mwana wa Ela alikuwa Kenasi. Wana wa Yehaleli walikuwa: Zifu, Sifa, Tiria na Asareli. Wana wa Ezra walikuwa: Yeteri, Meredi, Eferi na Yaloni. Meredi akamwoa Bitia, binti ya Mufalme wa Misri, na hawa ndio wana aliomuzalia Meredi: Miriamu, Samai na Isiba, mwanzilishi wa muji wa Estemoa. Meredi alikuwa na muke mwingine Muyuda. Huyu akamuzalia: Yeredi, mwanzilishi wa muji wa Gedori, Heberi, mwanzilishi wa muji wa Soko, na Yekutieli, mwanzilishi wa muji wa Zanoa. Hodia akaoa dada ya Nahamu ambaye wazao wake ndio waanzilishi wa: kabila la Garmi, lililoishi katika muji wa Keila; na kabila la Makati, lililoishi katika muji wa Estemoa. Wana wa Simoni walikuwa: Amunoni, Rina, Beni-Hanani na Tiloni. Isi alikuwa na wana wawili: Zoheti na Beni-Zoheti. Wana wa Sela mwana wa Yuda, walikuwa: Eri, mwanzilishi wa muji wa Leka; Lada, mwanzilishi wa muji wa Maresa, ukoo wa wafuma nguo za kitani waliokuwa wakiishi katika muji wa Beti-Asibea; Yokimu na watu walioishi katika muji wa Kozeba; na Yoasi na Sarafu waliotawala kule Moabu na wakarudia Lehemu. (Habari hizi ni za zamani sana.) Hawa ndio wafinyanzi walioishi katika miji ya Netaimu na Gedera, wakimutumikia mufalme. Simeoni alikuwa na wana watano: Nemueli, Yamina, Yaribu, Zera na Saulo. Walitawanyika mpaka kwenye mulango wa muji wa Gedori, upande wa mashariki wa bonde, kwa kuwatafutia kondoo wao malisho. Kule, walipata malisho tele, tena mazuri sana na tena inchi ilikuwa wazi, tulivu na yenye amani, maana wenyeji wa inchi hiyo wa zamani walikuwa wazao wa Hamu. Katika siku za utawala wa mufalme Hezekia wa Yuda, watu wale waliotajwa majina yao walikwenda kule Gedori, wakaharibu hema za Wameuni waliokuwa wakiishi kule na kuwafukuza kabisa mpaka leo. Wakafanya makao yao ya kudumu kule kwa sababu kulikuwa malisho tele kwa ajili ya kondoo wao. Watu wengine wa kabila la Simeoni yapata mia tano walikwenda mpaka kwenye mulima Seiri. Waliongozwa na Pelatia, Nearia, Refaya na Usieli, wana wa Isi. Kule wakawaua Waamaleki waliobaki kisha kuponyoka nao wakaishi kule mpaka leo. Hawa ndio wazao wa Rubeni, muzaliwa wa kwanza wa Israeli. (Ingawa Rubeni alikuwa muzaliwa wa kwanza haki yake ya muzaliwa wa kwanza ilipewa kwa ndugu yake Yosefu kwa sababu Rubeni alilala na habara wa baba yake. Kwa hiyo, yeye hakutiwa katika hesabu ya ukoo kulingana na haki yake ya muzaliwa wa kwanza. Ingawa kabila la Yuda ndilo lililokuja kuwa lenye nguvu zaidi kuliko mengine, na watawala walitoka mule, haki ya muzaliwa wa kwanza ilikuwa ya Yosefu). Wana wa Rubeni, muzaliwa wa kwanza wa Israeli, walikuwa: Hanoki, Palu, Hesironi na Karmi. Wazao wa Yoeli toka kizazi mpaka kizazi kingine walikuwa: Semaya, Gogo, Simei, Mika, Raya, Bali, na Bera, ambaye mufalme Tigilati-Pileseri wa Asuria, alimukamata mateka ingawa alikuwa kiongozi wa watu wa kabila la Rubeni, akamupeleka katika uhamisho. Wakubwa wa ukoo hizi ndio walioandikwa katika kitabu cha vizazi vya kabila la Rubeni: Yeieli, Zekaria, Bela mwana wa Ahazi na mujukuu wa Sema, wa ukoo wa Yoeli, uliokuwa ukiishi Aroeri na katika eneo lote la upande wa kaskazini mpaka Nebo na Bali-Meoni. Vilevile, kwa maana makundi yao ya nyama iliongezeka kwa wingi sana, walisambaa upande wa mashariki mpaka kwenye viingilio vya jangwa lililoenea mpaka kwenye muto Furati. Katika siku za utawala wa mufalme Saulo, kabila la Rubeni wakapigana vita na Wahagari, wakawaua katika vita na kutwaa inchi yao yote upande wa mashariki wa Gileadi, wakaishi mule. Kabila la Gadi lilikuwa na mupaka na kabila la Rubeni upande wa kaskazini, katika inchi ya Basani iliyoenea upande wa mashariki mpaka Saleka. Pale kulikuwa ukoo za: Yoeli, uliokuwa ukoo mukubwa zaidi; Safamu, ndio wa pili; Yanai; na Sefati kule Basani. Ndugu zao kulingana na ukoo zao walikuwa saba: Mikaili, Mesulamu, Seba, Yorai, Yakani, Zia na Eberi. Wote hawa walikuwa wana wa Abihaili, aliyekuwa mwana wa Huri. Huri alikuwa mwana wa Yaroa, Yaroa wa Gileadi, Gileadi wa Mikaili, Mikaili wa Yesisai, Yesisai wa Yado, na Yado wa Buzi. Ahi, aliyekuwa mwana wa Abudieli na mujukuu wa Guni, alikuwa mukubwa katika ukoo hizi. Waliishi katika sehemu ya Gileadi, katika Basani na miji yake na katika mashamba ya malisho yote ya Saroni, hata kwenye mipaka. Watu hao wote waliandikwa katika ukoo, katika siku za utawala wa Yotamu, mufalme wa Yuda, na Yeroboamu, mufalme wa Israeli. Makabila ya Rubeni, Gadi na Manase ya upande wa mashariki, yalikuwa na waaskari shujaa yapata elfu makumi ine na ine mia saba na makumi sita, wenye ngao na mapanga, wavuta pinde wafundi katika vita. Walipigana vita na makabila ya Wahagari, Yeturi, Nafisi na Nodabu. Waliweka tumaini lao kwa Mungu na wakamwomba awasaidie, naye akaitikia ombi lao na kuwatia katika mikono yao Wahagari pamoja na warafiki zao. Walinyanganya ngamia elfu makumi tano, kondoo elfu mia mbili na makumi tano, punda elfu mbili na kuwapeleka watu elfu mia moja kuwa wafungwa. Wakaua waadui wengi sana kwa sababu vita hiyo ilikuwa ni vita ya Mungu. Nao waliendelea kuishi katika inchi ile, mpaka wakati wa uhamisho. Nusu ya watu wa kabila la Manase waliishi katika inchi ya Basani. Hesabu yao iliongezeka kwa wingi sana, wakasambaa upande wa kaskazini mpaka Bali-Hermoni, Seniri na mulima Hermoni. Hawa ndio waliokuwa wakubwa wa ukoo za kabila lile: Eferi, Isi, Elieli, Azrieli, Yeremia, Hodavia na Yadieli. Wote walikuwa waaskari shujaa, watu wenye heshima sana na viongozi katika ukoo hizo. Lakini watu wakamwasi Mungu wa babu zao, wakafanya uzinzi kwa kuabudu miungu ya wakaaji wa inchi zile ambazo Mungu aliangamiza mbele yao. Basi, Mungu wa Israeli akasukuma roho ya Puli, mufalme wa Asuria, (ambaye alijulikana vilevile kwa jina la Tiglati-Pileseri), akashambulia inchi yao na kuwapeleka watu wa kabila la Rubeni, la Gadi na nusu ya kabila la Manase kwa upande wa mashariki mpaka uhamisho kule Hala, Habori na Hara, pembeni ya muto Gozani, ambako wamekaa mpaka leo. Lawi alikuwa na wana watatu: Gersoni, Kohati na Merari. Kohati alikuwa na wana wane: Amuramu, Izihari, Hebroni na Usieli. Yozadaki alikwenda katika uhamisho wakati Yawe alipowapeleka katika uhamisho watu wa inchi ya Yuda na Yerusalema kwa kutumia mukono wa mufalme Nebukadneza. Lawi alikuwa na wana watatu: Gersoni, Kohati na Merari. Wana wa Gersoni walikuwa: Libuni na Simei. Wana wa Kohati walikuwa: Amuramu, Izihari, Hebroni na Usieli. Wana wa Merari walikuwa: Mali na Musi. Hawa ndio wazao wa Lawi kufuatana na babu zao: Hawa ndio watu ambao mufalme Daudi aliweka kwa kazi ya kuimba katika nyumba ya Yawe, nyuma ya kuwekwa kwa Sanduku la Agano ndani yake. Walifanya kazi yao ya kuimba mbele ya hema takatifu la mukutano mpaka wakati mufalme Solomono alipojenga hekalu la Yawe kule Yerusalema. Walitumika kazi yao vizuri kufuatana na zamu ya kila kundi. Ndugu zao wengine walipewa kazi zingine katika hema takatifu la nyumba ya Mungu. Haruni na wazao wake ndio waliokuwa wakitoa sadaka juu ya mazabahu ya sadaka za kuteketezwa kwa moto na vilevile juu ya mazabahu ya kufukizia ubani. Walifanya kazi zote zilizoelekea Pahali Patakatifu Sana kwa kuifanyia Israeli upatanisho. Haya yote waliyafanya kulingana na maagizo Musa, mutumishi wa Mungu aliyotoa. Huu ndio urizi wao kulingana na mipaka yake: wazao wa Haruni katika jamaa ya Wakohati kulingana na kura yao, hao walipewa muji wa Hebroni katika inchi ya Yuda na mashamba ya malisho kandokando yake. Lakini mashamba katika muji pamoja na mashamba yake ya malisho yalitolewa kwa Kalebu mwana wa Yefune. Wazao wa Haruni wakapewa miji ya makimbilio: Hebroni, Libuna pamoja na mashamba yake ya malisho, Yatiri na Estemoa pamoja na mashamba yake ya malisho, Hileni na Debiri pamoja na mashamba yake ya malisho, Asani na Beti-Semesi pamoja na mashamba yake ya malisho. Katika eneo la kabila la Benjamina wakapewa miji ya Geba, Alemeti na Anatoti pamoja na malisho ya miji hiyo. Miji yote waliyopewa kulingana na jamaa zao ilikuwa kumi na mitatu. Miji kumi ya eneo la nusu ya kabila la Manase ilitolewa kwa sehemu iliyobaki ya ukoo wa Kohati kwa kura kulingana na jamaa zao. Ukoo wa Gersoni, kulingana na jamaa zake ulipewa miji kumi na mitatu katika kabila la Isakari, na katika kabila la Nafutali na katika kabila la Manase katika Basani. Vilevile, miji kumi na miwili katika kabila la Rubeni, na katika kabila la Gadi na katika kabila la Zebuluni ilipewa ukoo wa Merari kulingana na jamaa zao. Kwa njia hii watu wa Israeli waliwapa Walawi miji kusudi waishi ndani yake pamoja na mashamba ya malisho ya miji hiyo. (Miji iliyotajwa majina hapa juu katika kabila la Yuda, na katika kabila la Simeoni na katika kabila la Benjamina iligawanyiwa kwa kabila la Lawi kwa kura.) Jamaa zingine za ukoo wa Kohati zilipewa miji pamoja na malisho yake katika kabila la Efuraimu: Sekemu, muji wa makimbilio katika inchi ya milima ya Efuraimu pamoja na mashamba yake ya malisho, Gezeri pamoja na malisho yake, Yokimeamu pamoja na mashamba yake ya malisho, Beti-Horoni pamoja na mashamba ya malisho yake; Ayaloni pamoja na mashamba yake ya malisho, na Gati-Rimoni pamoja na mashamba yake ya malisho. Katika nusu ya kabila la Manase walipewa miji ya Aneri pamoja na mashamba yake ya malisho, na Bileamu pamoja na mashamba yake ya malisho. Hii ndiyo miji iliyopewa kwa jamaa za ukoo wa Kohati. Jamaa za ukoo wa Gersoni walipewa miji hii pamoja na mashamba yake ya malisho: katika nusu ya kabila la Manase walipewa: Golani katika Basani pamoja na mashamba yake ya malisho, Astaroti pamoja na mashamba yake ya malisho. Katika kabila la Isakari walipewa: Kedesi pamoja na mashamba yake ya malisho, Deberati pamoja na mashamba yake ya malisho, Ramoti pamoja na mashamba yake ya malisho na Anemu pamoja na malisho yake. Katika kabila la Aseri walipewa: Masali pamoja na mashamba yake ya malisho, Abudoni pamoja na mashamba yake ya malisho, Hukoki pamoja na mashamba yake ya malisho, na Rehobu na malisho yake. Katika kabila la Nafutali: Kedesi katika Galilaya pamoja na mashamba yake ya malisho, Hamoni pamoja na mashamba yake ya malisho na Kiriataimu pamoja na mashamba yake ya malisho. Jamaa za Merari zilizobakia, zilipewa miji hii pamoja na mashamba yake ya malisho kandokando ya miji hiyo. Katika kabila la Zebuluni walipewa Rimono pamoja na mashamba yake ya malisho na Tabori pamoja na mashamba yake ya malisho. Katika kabila Rubeni, upande wa mashariki ya muto Yordani karibu na muji wa Yeriko walipewa Bezeri unaokuwa katika inchi ya vilima pamoja na mashamba yake ya malisho, Yahasa pamoja na mashamba yake ya malisho, Kedemoti pamoja na mashamba yake ya malisho na Mefati pamoja na mashamba yake ya malisho. Katika kabila la Gadi walipewa Ramoti katika Gileadi pamoja na malisho yake, Mahanaimu pamoja na mashamba yake ya malisho, Hesiboni pamoja na mashamba yake ya malisho na Yazeri pamoja na mashamba yake ya malisho. Isakari alikuwa na wana wane: Tola, Pua, Yasubu na Simuroni. Wana wa Tola walikuwa: Usi, Refaya, Yerieli, Yamai, Ibusamu na Semweli. Hao walikuwa wakubwa wa jamaa za ukoo za Tola na watu mashujaa sana wa vita nyakati zao. Hesabu ya wazao wao siku za utawala wa mufalme Daudi ilikuwa elfu makumi mbili na mbili na mia sita. Mwana wa Usi alikuwa: Isirahia. Wana wa Isirahia walikuwa: Mikaeli, Obadia, Yoeli na Isia. Wote watano walikuwa wakubwa wa jamaa. Kwa vile wake na watoto wao walikuwa wengi sana, walikuwa na wanaume elfu makumi tatu na sita wanaoweza kuenda kwa vita. Ndugu zao katika jamaa zote za kabila la Isakari walioandikwa kwa kufuata ukoo, walikuwa elfu makumi munane na saba, na wote walikuwa mashujaa wa vita. Benjamina alikuwa na wana watatu: Bela, Bekeri na Yediaeli. Bela alikuwa na wana watano: Esiboni, Usi, Usieli, Yeremoti na Iri. Hawa walikuwa viongozi wa jamaa zao, na waaskari mashujaa. Walioandikwa kwa kufuata ukoo na hesabu ya wazao wao ilikuwa elfu makumi mbili na mbili na makumi tatu na wane. Wana wa Bekeri walikuwa: Zemira, Yoasi, Eliezeri, Eliehonai, Omuri, Yeremoti, Abiya, Anatoti na Alemeti. Wote hawa ni wazao wa Bekeri. Waliandikishwa kwa ukoo kulingana na vizazi vyao kama viongozi wa jamaa zao, na hesabu ya wazao wao ilikuwa elfu makumi mbili na mia mbili, wote wakiwa mashujaa wa vita. Mwana wa Yediaeli alikuwa: Bilihani. Wana wa Bilihani walikuwa: Yeusi, Benjamina, Ehudu, Kenana, Zetani, Tarsisi na Ahisahari. Wote hawa walikuwa wakubwa wa jamaa katika ukoo zao na waaskari mashujaa wa vita. Kutokana na wazao wao, kulipatikana wanaume elfu kumi na saba na mia mbili, waaskari hodari tayari kabisa kwa vita. Supimu na Hupimu walikuwa wana wa Iri. Husimu alikuwa mwana wa Aheri. Nafutali alikuwa na wana wane: Yazieli, Guni, Yereri na Salumu. Hao walikuwa wazao wa Biliha. Manase alikuwa na wana wawili kutoka kwa habara yake Mwaramu: Asirieli na Makiri. Makiri alikuwa baba ya Gileadi Makiri alizaa Hupimu na Supimu. Jina la dada yake lilikuwa Maka. Mwana wa pili wa Makiri aliitwa Zolofehadi. Zolofehadi alikuwa na wabinti peke yake. Maka muke wa Makiri, alizaa mwana jina lake Peresi. Jina la ndugu ya Peresi lilikuwa Seresi. Wana wa Seresi walikuwa Ulamu na Rakemu. Rakemu alizaa Bedani. Hawa wote ni wazao wa Gileadi, mwana wa Makiri, mujukuu wa Manase. Hamo-Leketi, dada ya Gileadi, alizaa: Isihodi, Abiezeri na Mala. Wana wa Semida walikuwa: Ahiana, Sekemu, Liki na Aniamu. Efuraimu baba yao aliomboleza vifo vyao kwa siku nyingi sana, na wandugu zake wakakuja kumufariji. Halafu Efuraimu akalala na muke wake, naye akapata mimba na kuzaa mwana. Efuraimu akamupa jina la Beria, kwa sababu ya magumu yaliyopata jamaa yake. Efuraimu alikuwa na binti jina lake Sera. Huyu ndiye aliyejenga miji ya Beti- Horoni ya juu na ya chini, na Uzeni-Sera. Inchi zao na makao yao yalikuwa: Beteli na vijiji vyake, muji wa Narani uliokuwa upande wa mashariki, muji wa Gezeri uliokuwa upande wa magaribi pamoja na vijiji vyake, Sekemu na vijiji vyake, na Aya na vijiji vyake. Na vilevile kwenye mipaka ya wana wa Manase: Beti-Seani na vijiji vyake, Tanaki na vijiji vyake, Megido na vijiji vyake na Dori na vijiji vyake. Hiyo ndiyo miji ambomo wazao wa Yosefu, mwana wa Israeli walimoishi. Wana wa Aseri walikuwa: Imuna, Isiwa, Isiwi na Beria, pamoja na binti mumoja jina lake Sera. Wana wa Beria walikuwa: Heberi na Malkieli, aliyekuwa baba ya watu wa muji wa Birza-Iti. Wana wa Heberi walikuwa: Yafuleti, Someri na Hotamu, na binti mumoja jina lake Sua. Wana wa Yafuleti walikuwa: Pasaki, Bimuhali na Asiwati. Wana wa Someri walikuwa: Roga, Yehuba, na Aramu. Wana wa Helemu walikuwa: Sofa, Imuna, Selesi na Amali. Wana wa Sofa walikuwa: Sua, Harneferi, Suali, Beri, Imura, Bezeri, Hodi, Sama, Silisa, Itirani na Bera. Wana wa Yeteri walikuwa: Yefune, Pisipa na Ara. Wana wa Ula walikuwa: Ara, Hanieli na Risia. Hao wote walikuwa wazao wa Aseri na walikuwa wakubwa wa jamaa zao, watu wafundi na hodari wa vita. Hesabu ya wale walioandikwa kwa kufuata ukoo katika kundi la waaskari ilikuwa elfu makumi mbili na sita. Benjamina alizaa wana hawa: Bela, muzaliwa wake wa kwanza; Asibeli, wa pili; Ahara, wa tatu; Noha, wa ine; na Rafa, wa tano. Wana wa Bela walikuwa: Adari, Gera, Abihudi, Abisua, Namani, Ahoa, Gera, Sefufanu na Huramu. Hawa ndio wazao wa Ehudu waliokuwa viongozi wa jamaa za wale waliokuwa wakiishi Geba, lakini wakapelekwa katika uhamisho kule Manahati: Namani, Ahiya na Gera. Gera, baba ya Uza na Ahihudi, ndiye aliyewaongoza walipohamishwa. Saharaimu alizaa watoto katika inchi ya Moabu, nyuma ya kufukuza wanawake wake Husimu na Bara. Kisha aliishi katika inchi ya Moabu, akamwoa Hodesi, naye akamuzalia wana hawa: Yoabu, Sibia, Mesa, Malakamu, Yeusi, Sakia, na Mirma. Hawa wana wake wote walikuja kuwa wakubwa wa ukoo. Husimu muke wa Saharaimu alimuzaliwa wana wengine wawili: Abitubu na Elipali. Wana wa Elipali walikuwa: Eberi, Misamu na Semedi ambaye alijenga miji ya Ono na Lodi, pamoja na vijiji kandokando yake; Beria na Sema walikuwa kati ya jamaa ambazo zilikuwa zinaishi katika muji wa Ayaloni, na kuwafukuza wenyeji wa Gati. Wana wa Beria walikuwa: Ahio, Sasaki, Yeremoti, Zebadia, Aradi, Ederi, Mikaeli, Isipa na Yoa. Hao ndio waliokuwa wakubwa wa ukoo zao kulingana na vizazi vyao. Walikuwa wanaishi Yerusalema. Yeieli alikuwa mwanzilishi wa muji wa Gibeoni. Muke wake aliitwa Maka. Muzaliwa wake wa kwanza alikuwa: Abudoni. Wana wake wengine walikuwa: Zuri, Kisi, Bali, Nadabu, Gedori, Ahio, Zekeri, na Mikiloti baba ya Simea. Hawa vilevile waliishi Yerusalema karibu na watu wengine wa ukoo wao. Neri alizaa Kisi, Kisi alizaa Saulo. Saulo alizaa: Yonatani, Malkisua, Abinadabu na Esibali. Mwana wa Yonatani alikuwa: Meribu-Bali; Meribu-Bali alizaa Mika. Wana wa Mika walikuwa: Pitoni, Meleki, Terea na Ahazi. Ahazi alizaa Yera. Naye Yera alizaa Alemeti, Azimaweti na Zimuri. Zimuri alizaa Moza. Moza alizaa Binea, Binea alizaa Rafa, aliyemuzaa Eleasa, naye Eleasa alizaa Azeli. Wana wa Azeli walikuwa: Azirikamu, Bokeru, Isimaeli, Searia, Obadia na Hanani. Wote hao walikuwa wana wa Azeli. Nao wana wa ndugu yake Eseki walikuwa: Ulamu, muzaliwa wake wa kwanza; Yeusi, wa pili; na Elifeleti wa tatu. Wana wa Ulamu walikuwa watu mashujaa sana wa vita, na wapiga upinde hodari. Alikuwa na wana na wajukuu wengi, jumla yao walikuwa mia moja makumi tano. Hao wote waliotajwa hapo juu walikuwa wa ukoo wa Benjamina. Hivi, Waisraeli wote walihesabiwa kufuatana na vizazi vyao na kuandikwa katika Kitabu cha Wafalme wa Israeli. Watu wa Yuda wamepelekwa katika utumwa mpaka Babeli kwa sababu ya kutokuwa waaminifu. Watu wa kwanza kurudia katika miji ya inchi yao walikuwa Waisraeli wa kawaida, makuhani, Walawi na watumishi wa hekalu. Wamoja kati ya watu wa makabila ya Yuda, Benjamina, ya Efuraimu na Manase walikwenda kuishi Yerusalema: Katika kabila la Yuda, kulikuwa: Utai mwana wa Amihudi na mujukuu wa Omuri. Naye Omuri alikuwa baba ya Imuri na mujukuu wa Bani, wa wazao wa Peresi mwana wa Yuda. Asaya wa uzao wa Silo, aliyekuwa muzaliwa wa kwanza wa jamaa yake, pamoja na wana wake. Yeuli wa uzao wa Zera. Watu wa kabila la Yuda waliokaa Yerusalema walikuwa mia sita na makumi kenda kwa jumla. Katika kabila la Benjamina, kulikuwa: Salu mwana wa Mesulamu mwana wa Hodavia mwana wa Hasenua, Ibuneya mwana wa Yerohamu, Ela mwana wa Usi mwana wa Mikiri, Mesulamu mwana wa Sefatia mwana wa Rueli mwana wa Ibunia. Watu hao walikuwa wakubwa wa ukoo zao. Watu wa kabila la Benjamina watu waliokaa Yerusalema walikuwa mia kenda na makumi tano na sita. Hawa ndio makuhani walioishi Yerusalema: Yedaya, Yoyaribu na Yakini, Azariya mwana wa Hilkia mwana wa Mesulamu mwana wa Zadoki, mwana wa Merayoti mwana wa Ahitubu, aliyekuwa mukubwa wa nyumba ya Mungu; na Adaya mwana wa Yerohamu mwana wa Pasuri mwana wa Malkia; na Masai mwana wa Adieli mwana wa Yazera mwana wa Mesulamu mwana wa Mesilemoti mwana wa Imeri. Wakubwa hawa wa ukoo za baba zao, pamoja na wandugu zao walikuwa kwa jumla watu elfu moja na mia saba na makumi sita. Walikuwa wakubwa wenye uwezo mukubwa katika kazi yote ya nyumba ya Mungu. Hawa ndio Walawi walioishi Yerusalema: Semaya, mwana wa Hasubu mwana wa Azirikamu mwana wa Hasabia, wa ukoo wa Merari; na Bakibakari, na Heresi, na Galali, Matania mwana wa Mika mwana wa Sikiri mwana wa Asafu; na Obadia mwana wa Semaya mwana wa Galali mwana wa Yedutuni; na Berekia mwana wa Asa mwana wa Elekana; waliokuwa wakiishi katika vijiji vya Wanetofati. Hawa ndio walinzi wa hekalu walioishi katika Yerusalema: Salumu, Akubu, Talmoni na Ahimani na wandugu zao. Salumu alikuwa mukubwa wao. Hata kufikia wakati ule, walinzi kutoka katika ukoo zao ndio waliolinda mulango wa mufalme wa upande wa mashariki. Zamani, walikuwa walinzi wa viingilio vya makambi ya Walawi. Salumu mwana wa Kore mwana wa Ebiasafu, pamoja na wandugu zake wa ukoo wa Kora, walikuwa na kazi ya kutunza viingilio vya hema la mukutano, kama vile babu zake walivyokuwa wakati wa ulinzi wa kambi ya Yawe. Finehasi mwana wa Eleazari, alikuwa musimamizi wao, zamani, Yawe alikuwa pamoja naye. Zekaria mwana wa Meselemia, alikuwa vilevile mulinzi wa viingilio vya hema la mukutano. Kwa jumla, watu mia mbili na kumi na wawili walichaguliwa kuwa walinzi wa viingilio vya hekalu. Waliandikwa kulingana na vijiji walimoishi. Mufalme Daudi na nabii Samweli ndio waliowaweka kwa kazi zao kwa sababu ya uaminifu wao. Basi, watu hao na wazao wao, waliendelea kulinda milango ya nyumba ya Yawe. Kila upande, ni kusema mashariki, magaribi, kaskazini na kusini, kulikuwa mulango uliokuwa na walinzi. Walinzi hawa walisaidiwa na wandugu zao waliokuwa wakiishi katika vijiji, ambao walilazimishwa kushika zamu ya ulinzi kwa muda wa siku saba, mara kwa mara, kwa maana wale walinzi wakubwa wane, ambao walikuwa Walawi, walikuwa na kazi ya kusimamia vyumba na hazina ya nyumba ya Mungu. Wao waliishi karibu na nyumba ya Mungu kwa sababu ilikuwa ni kazi yao kulinda na kufungua milango yake kila siku asubui. Walawi wengine walisimamia vyombo vilivyotumika wakati wa ibada. Walihitajika kuvihesabu wakati vilipotolewa na wakati viliporudishwa. Wengine walichaguliwa kusimamia vifaa vya hekalu, na vyombo vyote vitakatifu, na unga safi, divai, mafuta ya mizeituni, ubani na marasi. Lakini kazi ya kuchanga marasi ilifanywa na makuhani. Metitia, mumoja wa Walawi aliyekuwa muzaliwa wa kwanza wa Salumu, wa ukoo wa Kora, alisimamia utengenezaji wa sadaka ya mikate nyembamba. Nao wandugu zao wengine wa ukoo wa Kohati walikuwa na kazi ya kutayarisha mikate iliyotolewa kwa Mungu kila siku ya Sabato. Jamaa zingine za Walawi zilisimamia kazi ya nyimbo katika hekalu. Waliishi katika vyumba vimoja vya majengo ya nyumba ya Mungu na hawakuhitajika kufanya kazi ingine yoyote kwa maana walikuwa wakitumika usiku na muchana. Watu wote hawa waliotajwa walikuwa viongozi wa kabila la Walawi, kulingana na ukoo zao. Wao ndio viongozi walioishi Yerusalema. Yeieli alikuwa babu ya wakaaji wa muji wa Gibeoni ambamo aliishi yeye pamoja na muke wake aliyeitwa Maka. Muzaliwa wake wa kwanza aliitwa Abudoni, naye alifuatiwa na Zuri, Kisi, Bali, Neri, Nadabu, Gedori, Ahio, Zekaria na Mikloti. Mikiloti alizaa Simeamu. Wazao wao waliishi Yerusalema karibu na jamaa zingine za ukoo zao. Neri alizaa Kisi, naye Kisi alizaa Saulo. Saulo alikuwa na wana wane: Yonatani, Malikisua, Abinadabu na Esibali. Yonatani alizaa Meribu-Bali, Meribu-Bali alizaa Mika. Mika alikuwa na wana wane: Pitoni, Meleki, Tarea na Ahazi. Ahazi alizaa Yara, Yara alizaa Alemeti, Azimaweti na Zimuri, naye Zimuri alizaa Moza, Moza alizaa Binea, Binea alizaa Refaya, Refaya alizaa Eleasa, naye Eleasa alizaa Aseli. Aseli alikuwa na wana sita: Azirikamu, Bokeru, Isimaeli, Searia, Obadia na Hamani. Hawa wote walikuwa wana wa Aseli. Siku moja, Wafilistini wakapigana vita na Waisraeli; nao Waisraeli wakakimbia mbele ya Wafilistini na kuuawa katika mulima wa Gilboa. Lakini Wafilistini wakamuzunguka Saulo na wana wake, kisha wakawaua Yonatani, Abinadabu na Malikisua wana wa Saulo. Vita ilikuwa kali sana juu ya Saulo. Wapiga mishale walipomwona wakamwumiza sana. Kwa hiyo Saulo akamwambia mutu aliyemubebea silaha: “Chomoa upanga wako unichome nikufe, kusudi watu hawa wasiotahiriwa wasikuje kunichekelea.” Lakini yule aliyemubebea silaha hakutaka kufanya vile; aliogopa sana. Halafu, Saulo alitwaa upanga wake mwenyewe akauangukia. Wakati yule aliyemubebea silaha alipoona kwamba Saulo amekufa, naye vilevile akauangukia upanga wake, akakufa. Hivi ndivyo Saulo alivyokufa, yeye na wana wake watatu, na jamaa yake yote. Nao watu wa Israeli walioishi katika bonde walipoona waaskari wamekimbia waadui, na kwamba Saulo na wana wake wamekufa, wakahama toka miji yao, wakakimbia. Wafilistini wakaenda na kukaa katika miji hiyo. Kesho yake, Wafilistini walipokwenda kutwaa vitu vya wale waliouawa, wakakuta maiti ya Saulo na wana wake kwenye mulima Gilboa. Wakamvua nguo, wakatwaa kichwa chake pamoja na silaha zake, halafu wakatuma wajumbe katika inchi yote ya Filistia kutangaza habari kwa sanamu zao na watu. Wakaweka silaha za Saulo katika hekalu la miungu yao, kisha wakatundika kichwa chake katika hekalu la Dagoni. Lakini watu wa Yebesi Gileadi waliposikia yote Wafilistini waliyomutendea Saulo, mashujaa wote wakaondoka na kutwaa mwili wa Saulo na miili ya wana wake, wakaileta mpaka Yabesi. Wakazika mifupa yao chini ya muti wa mwalo kule Yabesi, nao wakafunga kula kwa muda wa siku saba. Saulo alikufa kwa sababu ya kutokuwa mwaminifu; hakukuwa mwaminifu maana hakutii neno la Yawe na alikwenda kwa mwaguzi kumwomba shauri, pahali pa kumwendea Yawe kwa kumwomba shauri. Kwa sababu hiyo Yawe akamwua, na akamupa Daudi mwana wa Yese ufalme wake. Kisha Waisraeli wote walikusanyika mbele ya Daudi kule Hebroni, wakamwambia: “Sisi ni mwili na damu yako. Zamani, Saulo alipokuwa mufalme wewe ndiwe uliyewaongoza Waisraeli katika vita, na Yawe, Mungu wako alikuambia: ‘Utakuwa muchungaji wa watu wangu Waisraeli, na utakuwa mukubwa wa watu wangu Waisraeli.’ ” Basi, wazee wote wa Waisraeli wakamwendea mufalme kule Hebroni; naye Daudi akafanya agano nao mbele ya Yawe, halafu wakamupakaa Daudi mafuta akuwe mufalme wa Waisraeli kulingana na neno la Yawe lililotolewa kwa njia ya Samweli. Nyuma ya hayo Daudi na Waisraeli wote walikwenda Yerusalema, muji uliojulikana kwa jina la Yebusi, na ambao wenyeji wake walikuwa Wayebusi. Wakaaji wa Yebusi wakamwambia Daudi: “Hautaingia katika muji huu.” Hata hivyo, Daudi akanyanganya makimbilio ya Sayuni, ni kusema muji wa Daudi. Halafu Daudi akasema: “Mutu atakayetangulia kuwapiga Wayebusi, atakuwa mukubwa na jemadari katika jeshi.” Basi Yoabu mwana wa Zeruya, akakuwa wa kwanza kuwashambulia, hivyo akakuwa mukubwa. Daudi alikaa katika makimbilio yale, na kwa hiyo, muji ule ukaitwa “Muji wa Daudi.” Akajenga muji ule, akianzia uwanja wa Milo, na kuuzunguka wote, na Yoabu akatengeneza muji ule upya. Naye Daudi akazidi kuwa mukubwa kwa sababu Yawe wa majeshi alikuwa pamoja naye. Haya ndiyo majina ya wakubwa wa mashujaa wa Daudi, ambao pamoja na watu wengine wote wa Israeli, walimwunga mukono kwa pamoja kusudi akuwe mufalme, sawa na neno Yawe alilotoa juu ya Waisraeli. Haya ndiyo majina ya mashujaa wale wa Daudi: Yasobeamu, wa ukoo wa Hakemoni, aliyekuwa kiongozi wa “Wale makumi tatu.” Yeye alipigana kwa mukuki wake akaua watu mia tatu kwa mara moja katika vita. Halafu aliyefuata kati ya wale mashujaa watatu alikuwa Eleazari mwana wa Dodo, wa ukoo wa Ahoa. Siku moja Eleazari alikuwa pamoja na Daudi kule Pasi-Damimu, wakati Wafilistini walipokusanyika kupigana vita. Kule kulikuwa shamba lenye shayiri tele, lakini Waisraeli wakawakimbia Wafilistini. Lakini wakasimama imara katikati ya shamba lile kwa kulikinga, wakaua Wafilistini; Yawe akawaokoa kwa kuwapa ushindi mukubwa. Kisha mashujaa watatu kati ya wakubwa makumi tatu wakamwendea Daudi kwenye mulima wa pango la Adulamu. Wakati ule jeshi la Wafilistini lilikuwa limepiga kambi katika bonde la Refaimu. Naye Daudi wakati ule alikuwa katika maficho, nalo jeshi la Wafilistini lilikuwa katika muji wa Betelehemu. Daudi akapatwa na hamu kubwa akasema: “Heri kama mutu angeweza kunipa maji ya kunywa kutoka katika kisima cha Betelehemu kinachokuwa karibu na mulango wa muji!” Wale mashujaa wake watatu wakatoka, wakapenya katikati ya kambi ya jeshi la Wafilistini, wakaenda na kuchota maji katika kisima cha Betelehemu, karibu na mulango wa muji, wakamuletea Daudi. Lakini Daudi akakataa kuyakunywa, na kwa pahali pake akayamwanga chini kama sadaka kwa Yawe akisema: “Tendo kama hili lipite mbali nami; siwezi kulifanya mbele ya Mungu wangu. Basi ninaweza kunywa damu ya maisha ya watu hawa? Maana kwa kuyahatarisha maisha yao walileta maji haya.” Kwa hiyo Daudi hakukunywa maji yale. Hayo ndiyo mambo waliyotenda wale mashujaa watatu. Abisai, ndugu ya Yoabu, alikuwa mukubwa wa mashujaa makumi tatu. Yeye alipigana kwa mukuki wake na watu mia tatu, akawaua, akajipatia jina kati ya wale mashujaa watatu. Basi, akaheshimiwa zaidi kati ya mashujaa makumi tatu, hata akakuwa jemadari wao, lakini hakukuwa shujaa kama wale mashujaa watatu. Benaya mwana wa Yehoyada, kutoka muji wa Kabuseli, alikuwa askari shujaa ambaye alifanya mambo mengi ya ajabu. Aliua mashujaa wawili kutoka Moabu, na siku moja wakati wa baridi kali, akashuka na kuua simba ndani ya shimo. Vilevile, akamwua Mumisri mumoja, urefu wake ulikuwa metre mbili na nusu, naye alikuwa akibeba mukuki mukubwa sana katika mukono wake, kama muti wa mufumaji wa nguo. Lakini Benaya akamushambulia akiwa na fimbo tu, akamunyanganya mukuki ule, na kumwua Mumisri yule kwa mukuki wake mwenyewe. Benaya mwana wa Yehoyada alifanya mambo hayo, akajipatia sifa kati ya wale mashujaa watatu. Basi, akakuwa mwenye heshima kati ya wale mashujaa makumi tatu, ingawa hakukuwa shujaa kama wale mashujaa watatu. Na Daudi akamupa cheo cha mukubwa wa walinzi wake wa kipekee. Hawa ndio wanaume ambao walijiunga na Daudi kule Ziklagi, alipokuwa hana uhuru wowote wa kutembea kwa sababu ya mufalme Saulo mwana wa Kisi. Watu hawa walikuwa kati ya waaskari mashujaa waliomusaidia katika vita. Walikuwa wa kabila la Benjamina kama vile Saulo alivyokuwa. Walikuwa wapiga upinde hodari, na warusha mawe hodari kwa kutumia mikono yote, wa kuume na wa kushoto. Haya ndiyo majina yao: Hao watu wa kabila la Gadi walikuwa wakubwa wa waaskari. Kulingana na vyeo vyao, mudogo alisimamia kundi la waaskari mia moja, na mukubwa alisimamia kundi la waaskari elfu moja. Hawa ndio watu waliovuka muto Yordani katika mwezi wa kwanza, muto ulipokuwa umefurika pande zote na kuwatawanya watu kwa upande wa mashariki na magaribi ya muto. Watu wamoja wa makabila ya Benjamina na Yuda wakafika pahali Daudi alipokuwa akijificha. Daudi akatoka inje kwa kuwapokea, akawaambia: “Ikiwa mumekuja kwangu kama warafiki kwa kunisaidia basi ninawapokea kwa moyo wote, lakini kama mumekuja kwa kunitoa kwa waadui zangu, ingawa sijatenda ovu lolote, Mungu wa babu zetu awaone na kuwaazibu ninyi.” Halafu Roho akamujaza Amasai, mukubwa wa wale watu makumi tatu, naye akasema: “Sisi ni watu wako, ee Daudi! Tuko upande wako, ee mwana wa Yese! Amani, amani ikuwe kwako, na amani ikuwe kwa yeyote anayekusaidia! Maana Mungu wako ndiye anayekusaidia.” Kisha Daudi akawapokea na kuwafanya wakubwa katika kundi lake. Waaskari wengine wa kabila la Manase, wakatoroka na kwenda kujiunga na Daudi, wakati alipoondoka pamoja na Wafilistini kwenda kupigana na mufalme Saulo. (Lakini hata hivyo, hakuwasaidia maana watawala wa Wafilistini walifanya shauri wamufukuze arudie Ziklagi wakisema: “Tutahatarisa maisha yetu kwa sababu atatutoroka na kurudia kwa bwana wake Saulo.”) Basi, Daudi alipokuwa Ziklagi, watu hawa wa kabila la Manase wakamwendea: Adina, Yozabadi, Yediaeli, Mikaeli, Yozabadi, Elihu na Siletayi. Kila mumoja wao alikuwa kiongozi wa kundi la watu elfu moja katika kabila la Manase. Wakamusaidia Daudi kupigana na makundi ya washambulizi, maana wote walikuwa waaskari mashujaa na majemadari wa waaskari. Siku kwa siku, watu walijiunga na Daudi kwa kumusaidia, na nyuma akakuwa na kundi kubwa sana la waaskari, kama jeshi la Mungu. Hii ndiyo hesabu ya makundi ya waaskari wenye silaha waliojiunga na Daudi kule Hebroni kwa kumutwalia ufalme kutoka kwa Saulo, kulingana na neno la Yawe: Watu wa kabila la Yuda waliokuwa na mikuki na ngao, walikuwa elfu sita na mia nane. Wote walikuwa na silaha zao. Kutoka kabila la Simeoni, watu elfu saba na mia moja mashujaa na wenye ujuzi mwingi wa vita. Kutoka kabila la Lawi: watu elfu ine na mia sita. Yehoyada, wa uzao wa Haruni na wenzake: watu elfu tatu na mia saba. Jamaa za Zadoki, kijana hodari katika vita, yeye pamoja na majemadari makumi mbili na wawili kutoka ukoo wa baba yake mwenyewe. Kutoka kabila la Benjamina, (kabila la Saulo): watu elfu tatu. Wengi wao walibaki waaminifu kwa jamaa ya Saulo. Kutoka kabila la Efuraimu: watu elfu makumi mbili na mia nane, watu mashujaa sana tena waliheshimiwa katika ukoo zao. Kutoka nusu ya kabila la Manase: watu elfu kumi na nane, waliotajwa majina kwa kuja kumuweka Daudi kuwa mufalme. Kutoka kabila la Isakari: wakubwa mia mbili pamoja na wandugu zao wote waliokuwa chini ya waangozi wao. Wakubwa hao walikuwa na elimu ya kujua mambo ya nyakati na walijua mambo Waisraeli waliyopasha kufanya. Kutoka kabila la Zebuluni: watu elfu makumi tano; waaminifu na wanaoelewa wa vita. Wakajitayarisha na silaha za vita za kila namna, shabaha yao ilikuwa ni kumusaidia Daudi tu. Kutoka kabila la Nafutali: majemadari elfu moja pamoja na watu elfu makumi tatu na saba wenye ngao na mikuki. Kutoka kabila la Dani: watu elfu makumi mbili na nane mia sita wenye silaha tayari kwa vita. Kutoka kabila la Aseri: watu elfu makumi ine wenye kuelewa vita, tayari kwa mapigano. Kutoka kabila la Rubeni, Gadi na nusu ya kabila la Manase kutoka ngambo ya muto Yordani: watu elfu mia moja na makumi mbili wenye kila aina ya silaha za vita. Waaskari hao wote, waliojitayarisha kabisa kwa vita, walikwenda Hebroni na nia yao kubwa ikiwa ni kumuweka Daudi kuwa mufalme wa inchi yote ya Israeli. Nao watu wote wa Israeli, wakaungana wakiwa na nia moja ya kumuweka Daudi kuwa mufalme. Basi, walikaa na Daudi kwa muda wa siku tatu, wakikula na kunywa maana wandugu zao walikuwa wamekwisha kuwatayarishia vyakula. Zaidi ya hayo, wajirani zao wa karibu na hata wa mbali kama kule Isakari, Zebuluni na Nafutali, waliwaletea vyakula walivyobeba juu ya punda, ngamia, nyumbu na ngombe. Waliwaletea unga, mikate ya tini, zabibu zenye kukauka, divai na mafuta, ngombe na kondoo wengi, kukakuwa vyakula tele, maana kulikuwa furaha katika inchi ya Israeli. Daudi akashauriana na majemadari wa makundi ya maelfu na makundi ya mamia, pamoja na viongozi wote. Kisha akawaambia Waisraeli wote waliokusanyika: “Ikiwa mutakubaliana nami, na ikiwa ni mapenzi ya Yawe, Mungu wetu, tufanye hivi: tutume wajumbe waende wawaite wandugu zetu waliobaki katika inchi ya Israeli, pamoja na makuhani na Walawi wanaokuwa katika miji yao na mashamba ya malisho yao, wakuje kukusanyika pamoja nasi. Kisha tuende tukamate Sanduku la Agano la Mungu wetu, maana hatukulijali wakati wa utawala wa mufalme Saulo.” Watu wote wakakubaliana na pendekezo lile maana waliliona kuwa jambo jema. Kwa hiyo, Daudi akawakusanya Waisraeli wote katika inchi, tokea kwenye kijito cha Sihori kinachokuwa Misri, mpaka kwenye kiingilio cha Hamati kwa kulileta Sanduku la Agano toka Kiriati-Yearimu. Daudi akiandamana na Waisraeli wote, akaenda mpaka katika muji wa Bala, ni kusema Kiriati-Yearimu, katika inchi ya Yudea, kwa kulitwaa toka kule Sanduku la Agano linaloitwa kwa jina la Yawe anayeikaa kwenye kiti chake cha kifalme juu ya makerubi. Basi, wakalitwaa Sanduku la Agano kutoka katika nyumba ya Abinadabu wakilibeba juu ya gari jipya. Uza na Ahio wakaongoza gari lile. Daudi na Waisraeli wote wakakuwa wanacheza kwa nguvu zao zote, mbele ya Mungu. Waliimba nao wakikuwa wanapiga ala za muziki zilizotengenezwa kwa muti wa muvinje: vinubi, vinanda, matari, matoazi na baragumu. Walipofika kwenye uwanja wa kupepetea ngano wa Kidoni, Uza akaunyoosha mukono wake kwa kuzuia Sanduku la Agano kwa sababu ngombe walijikwaa. Mara moja Yawe akamukasirikia Uza kwa kuligusa sanduku, akamwua. Uza akakufa palepale mbele ya Mungu. Daudi akakasirika kwa sababu Yawe alimwua Uza akiwa na hasira. Kwa sababu hiyo, pahali pale panaitwa Pigo la Uza mpaka leo. Siku hiyo Daudi akamwogopa Mungu, akasema: “Sasa, nitaweza namna gani kupeleka Sanduku la Agano katika nyumba yangu?” Basi, Daudi hakupeleka sanduku mpaka katika muji wa Daudi, lakini akalipeleka katika nyumba ya Obedi-Edomu wa Gati. Sanduku lile la Mungu lilikaa kule kwa Obedi-Edomu kwa muda wa miezi mitatu, naye Yawe akabariki nyumba ya Obedi-Edomu na mali yake yote. Kisha mufalme Hiramu wa Tiro akatuma wajumbe kwa Daudi, akamupelekea vilevile miti ya mierezi, wajengaji na waseremala, kusudi wamujengee Daudi nyumba ya kifalme. Halafu, Daudi akatambua kwamba Yawe amemwimarisha akuwe mufalme wa Israeli, na kwamba ufalme wake umetukuzwa kwa ajili ya Waisraeli, watu wake. Kule Yerusalema, Daudi akaoa wake wengi zaidi, naye alizaa wana na wabinti wengine. Haya ndiyo majina ya watoto aliozaa kule Yerusalema: Samua, Sobabu, Natani, Solomono, Ibuhari, Elisua, Elipeleti, Noga, Nefegi, Yafia, Elisama, Beliada na Elifeleti. Wafilistini waliposikia kwamba Daudi amepakwa mafuta kuwa mufalme wa inchi nzima ya Waisraeli, wote wakatoka kwa wingi kwenda kumutafuta. Daudi alipopata habari, akatoka kwenda kupigana nao. Wafilistini wakafika wakaanza mashambulizi katika bonde la Refaimu. Halafu Daudi akamwomba Mungu shauri: “Niende kuwashambulia Wafilistini? Utawatia katika mikono yangu?” Naye Yawe akamwambia: “Kwenda, nitawatia katika mikono yako.” Basi, Daudi akaenda kule Bali-Perasimu, akawashinda; halafu akasema: “Mungu amebomoa ukingo wa waadui zangu kwa mukono wangu, kama mafuriko ya maji yanayoenda mbio.” Kwa hiyo pahali pale panaitwa “Bwana Mwenye Kubomoa.” Wafilistini walipokimbia, waliacha sanamu za miungu yao kule, naye Daudi akatoa amri zote zichomwe kwa moto. Kisha Wafilistini wakafanya mashambulizi katika bonde lile kwa mara ya pili. Mara hii, Daudi alipoomba shauri kwa Mungu, Mungu akamwambia: “Usiwashambulie kutokea hapa, lakini zunguka nyuma yao na kuwashambulia kutokea mbele ya miti ya miforosadi, halafu uwashambulie kutokea kule. Na mara moja utakaposikia vishindo vya miguu kwenye vilele vya ile miforosadi, halafu, toka uende katika vita. Nitakuwa nimekwisha kukutangulia kuwapiga waaskari wa Wafilistini.” Daudi akafanya kama vile alivyoamuriwa na Mungu. Akawapiga waaskari wa Wafilistini kutokea Gibeoni mpaka Gezeri. Daudi akakuwa na sifa popote katika inchi, naye Yawe akayatia hofu mataifa yote, nayo yakamwogopa sana. Daudi akajengea nyumba katika muji wa Daudi. Tena akatengenezea Sanduku la Agano nafasi, akalipigia hema. Kisha akasema: “Hakuna mutu mwingine yeyote atakayebeba Sanduku la Agano isipokuwa Walawi, maana Yawe aliwachagua wao kwa kulibeba na kumutumikia kwa milele.” Basi, akawakusanya Waisraeli wote wakuje Yerusalema, kwa kuleta Sanduku la Agano la Yawe pahali alipolitayarishia. Daudi akawaita makuhani wawili, Zadoki na Abiatari, na Walawi sita, Urieli, Asaya, Yoeli, Semaya, Elieli na Aminadabu; akawaambia: “Ninyi ni viongozi wa ukoo za Walawi. Mujitakase pamoja na wandugu zenu, mupate kuleta Sanduku la Agano la Yawe, Mungu wa Israeli, mpaka pahali ambapo nimelitayarishia. Kwa sababu hamukulibeba safari ya kwanza, Yawe, Mungu wetu, akatuazibu maana hatukulitunza kama vile alivyoagiza.” Basi, makuhani na Walawi wakajitakasa kusudi wapate kuleta Sanduku la Agano la Yawe, Mungu wa Israeli. Walawi wakalibeba juu ya mabega yao wakitumia miti yake ya kuibebea kama Musa alivyoamuru, kulingana na neno la Yawe. Daudi aliwaamuru vilevile wakubwa wa Walawi wachague kati ya wandugu zao waimbaji wakuwe wanaimba na kupiga ala za muziki kwa nguvu, kwa kutoa sauti za furaha. Walipiga vinanda, vinubi na matoazi. Hivyo wakachagua watu hawa katika ukoo za waimbaji: Hemani mwana wa Yoeli, ndugu yake Asafu aliyekuwa mwana wa Berekia na wana wa Merari, ndugu zao, na Etani mwana wa Kusaya. Kisha wakawachagua Walawi hawa wakuwe wasaidizi wao kwa kushika nafasi ya pili: Zekaria, Yazieli, Semiramoti, Yehieli, Uni, Eliabu, Benaya, Maseya, Matitia, Elifelehu na Mikineya na walinzi wa mulango: Obedi-Edomu na Yeieli. Hemani, Asafu na Etani wakachaguliwa kupiga matoazi ya shaba. Zekaria, Azieli, Semiramoti, Yehieli, Uni, Eliabu, Maseya na Benaya, walikuwa wapiga vinubi vya sauti ya juu. Matitia, Elifelehu, Mikineya, Obedi-Edomu, Yeieli na Azazia waliongoza wakiwa na vinubi vya sauti ya chini. Naye Kenania kwa sababu ya ujuzi wa muziki aliokuwa nao, aliwekwa kuwa kiongozi wa wote. Berekia na Elekana walikuwa walinzi wa Sanduku la Agano. Sebania, Yosafati, Netaneli, Amasai, Zekaria, Benaya na Eliezeri, waliokuwa makuhani, waliwekwa kwa kupiga baragumu mbele ya Sanduku la Agano. Obedi-Edomu na Yehiya waliwekwa vilevile kuwa walinzi wa sanduku. Basi, Daudi, wazee wa Waisraeli na majemadari wa maelfu, wakaenda kutwaa Sanduku la Agano la Yawe kutoka katika nyumba ya Obedi-Edomu kwa shangwe. Wakamutolea Mungu sadaka: ngombe dume saba na kondoo dume saba kwa sababu aliwasaidia wale Walawi waliolibeba Sanduku la Agano la Yawe. Daudi alikuwa akivaa kanzu ya kitani safi, hata vilevile na Walawi wote waliobeba sanduku, waimbaji na Kenania kiongozi wa waimbaji. Zaidi ya kanzu ile, Daudi alikuwa akivaa kizibao cha kitani. Hivyo, Waisraeli wote wakakusanyika pamoja kwa shangwe kwa kubeba Sanduku la Agano la Yawe mpaka Yerusalema. Wakalisindikiza kwa mulio wa baragumu, ngunga, matoazi, na sauti kubwa za vinanda na vinubi. Sanduku la Agano la Yawe lilipokuwa likiingia katika muji wa Daudi, Mikali, binti wa Saulo, akachungulia kwenye dirisha, akamwona mufalme Daudi akicheza na kushangilia, basi akamuzarau ndani ya moyo wake. Kisha wakaingiza Sanduku la Agano, na kuliweka ndani ya hema ambayo Daudi alikuwa ametayarisha. Halafu wakatoa sadaka za kuteketezwa kwa moto na za amani mbele ya Mungu. Daudi alipomaliza kutoa sadaka hizo za kuteketezwa na za amani, akawabariki watu katika jina la Yawe, na akawagawanyia Waisraeli wote, wanaume na wanawake, kila mumoja akapewa mukate, kipande cha nyama na mukate wa zabibu. Zaidi ya hayo, Daudi akaweka Walawi wamoja kwa kazi mbele ya Sanduku la Agano la Yawe, wamutukuze, wamutolee shukrani na wamusifu Yawe, Mungu wa Israeli. Akamuchagua Asafu kuwa kiongozi wao, akisaidiwa na Zekaria. Yeieli, Semiramoti, Yehieli, Metitia, Eliabu, Benaya, Obedi-Edomu na Yehieli, akawachagua wakuwe wapiga vinanda na vinubi. Asafu alipiga matoazi, nao makuhani Benania na Yaharieli, wakachaguliwa wakuwe wakipiga baragumu kwa mufululizo mbele ya Sanduku la Agano la Mungu. Basi, hiyo ikakuwa siku ambayo kwa mara ya kwanza, Daudi alimupa Asafu na wandugu zake Walawi kazi ya kumwimbia Yawe nyimbo za shukrani. Mutangaze ukubwa wa Yawe, mujulishe mataifa mambo aliyoyatenda! Mushangilie, mumwimbie Mungu sifa; mueleze matendo yake ya ajabu! Mujisifu kwa ajili ya jina lake takatifu; wanaomutafuta Yawe wafurahi. Mumutafute Yawe mwenye nguvu; mumutafute Yawe siku zote. Mukumbuke matendo ya ajabu aliyotenda, maajabu yake na hukumu alizotoa, enyi wazao wa Abrahamu, mutumishi wake, enyi wazao wa Yakobo, wachaguliwa wake. Yeye Yawe, ndiye Mungu wetu; hukumu zake zina nguvu katika dunia yote. Yeye anashika agano lake milele, anatimiza ahadi zake kwa vizazi elfu. Anashika agano alilofanya na Abrahamu, na ahadi aliyomwapia Isaka. Alimusimamishia Yakobo ahadi yake, akamuhakikishia agano hilo la milele. Alisema: “Nitawapa inchi ya Kanana, nayo itakuwa mali yenu wenyewe.” Hesabu yenu ilikuwa ndogo, mulikuwa wachache na wageni katika inchi ya Kanana, mukitangatanga toka taifa hata taifa, kutoka inchi moja hata inchi ingine. Mungu hakumuruhusu mutu yeyote awatese; kwa ajili yao aliwaonya wafalme: “Musiwaguse wachaguliwa wangu; musiwazuru manabii wangu!” Mumwimbie Yawe, ulimwengu wote. Mutangaze kila siku matendo yake ya wokovu. Mutangazie mataifa utukufu wake, muwaelezee watu wote matendo yake ya ajabu. Maana Yawe ni mukubwa, anasifika sana anastahili kuheshimiwa kuliko miungu yote. Miungu yote ya mataifa mengine si kitu; lakini Yawe ndiye aliyeumba mbingu. Utukufu na sifa vinamuzunguka, nguvu na furaha vinajaza pahali pake. Mumupe Yawe heshima, enyi jamii zote za watu, mutangaze utukufu na nguvu yake. Mumupe Yawe heshima ya utukufu wa jina lake; mulete sadaka na kuingia katika nyumba yake. Mumwabudu Yawe katika Pahali Patakatifu pake. Ee dunia yote; tetemeka mbele yake! Ameweka ulimwengu imara, hautatikisika. Mufurahi enyi mbingu na dunia! Muambie mataifa: “Yawe anatawala!” Bahari ivume, pamoja na vyote vinavyokuwa mule! Mufurahi enyi mashamba na vyote vinavyokuwa mule! Halafu miti yote katika pori itaimba kwa furaha mbele ya Yawe anayekuja kuihukumu dunia. Mumushukuru Yawe! Yeye ni muzuri, wema wake unadumu milele! Mumwambie Yawe: utuokoe, ee Mungu wa wokovu wetu, utukusanye pamoja na kutuokoa kutoka kwa mataifa, tupate kulisifu jina lako takatifu, kuona utukufu juu ya sifa zako. Asifiwe Yawe, Mungu wa Israeli, tangu milele na hata milele! Kisha watu wote wakasema: “Amina!” Wakamusifu Yawe vilevile. Halafu, mufalme Daudi akawaacha Asafu na wandugu zake Walawi pahali walipoliweka Sanduku la Agano la Yawe, kwa ajili ya kazi zinazotakiwa mbele ya sanduku kila siku. Obedi-Edomu mwana wa Yedutuni, pamoja na wenzake makumi sita na wanane waliwasaidia. Obedi-Edomu mwana wa Yedutuni na Hosa walikuwa walinzi wa milango. Mufalme Daudi akawaweka kuhani Zadoki na makuhani wenzake kuwa watumishi wa hema ya Yawe iliyokuwa pahali pa kuabudia kule Gibeoni kwa kutolea Yawe sadaka za kuteketezwa kwa moto juu ya mazabahu ya sadaka za kuteketezwa kwa moto siku zote asubui na magaribi, kulingana na yote yaliyoandikwa katika sheria ambayo Yawe aliyowaamuru Waisraeli. Pamoja nao kulikuwa Hemani na Yedutuni na wale wote waliochaguliwa, waliotajwa majina yao, kwa kumushukuru Yawe kwa sababu wema wake unadumu milele. Hemani na Yedutuni walikuwa na baragumu na matoazi kwa ajili ya muziki na ala za muziki kwa ajili ya nyimbo takatifu. Wana wa Yedutuni walichaguliwa kwa kulinda milango. Kisha, kila mutu akaondoka kwenda kwake; naye Daudi akaenda kwake kwa kuibariki jamaa yake. Wakati mufalme Daudi alipokuwa akiikaa katika nyumba yake ya kifalme, siku moja akamwita nabii Natani, na kumwambia: “Angalia, mimi ninakaa katika nyumba nzuri iliyojengwa na miti ya mwerezi, lakini Sanduku la Agano la Yawe linakaa ndani ya hema.” Natani akamwambia Daudi: “Ufanye chochote unachofikiri ndani ya moyo wako, maana Mungu yuko pamoja nawe.” Lakini usiku uleule, neno la Yawe lilimufikia Natani kusema hivi: “Kwenda umwambie mutumishi wangu Daudi: Yawe anasema hivi: Wewe hautanijengea nyumba ya kukaa. Tangu wakati ule nilipowaongoza watu wa Israeli kutoka Misri mpaka hivi leo, sijaishi katika nyumba. Nimekuwa nikihama toka hema hata hema, na toka makao hata makao mengine. Kila pahali nilipokwenda na Waisraeli, sikupata hata mara moja kuwauliza waamuzi wao niliowaamuru wachunge watu wangu, ‘Kwa nini haukunijengea nyumba ya mierezi?’ “Kwa hiyo basi, umwambie mutumishi wangu Daudi: Yawe wa majeshi anasema hivi: Nilikutoa katika shamba la malisho ulipokuwa unachunga kondoo, kusudi ukuwe mukubwa wa watu wangu Waisraeli. Tangu wakati ule nimekuwa pamoja nawe kokote ulikokwenda na nimewaangamiza waadui zako wote mbele yako. Nitakufanya kuwa mwenye heshima kama vile wakubwa wengine wa dunia. Nami nitawachagulia watu wangu wa Israeli pahali pa kuishi niwapandikize, kusudi waishi pahali pao wenyewe, wasisumbuliwe tena. Nao watu wakali wanaotumia nguvu hawatawatesa tena kama zamani, wakati nilipowachagua waamuzi juu ya watu wangu Waisraeli. Mimi nitawashinda waadui zako wote. Zaidi ya yote, mimi Yawe ninakutangazia kwamba nitakupa wazao. Siku zako zitakapotimia za kujiunga na babu zako, nitamufanya mumoja wa watoto wako wewe mwenyewe akuwe mufalme; nami nitaimarisha ufalme wake. Yeye ndiye atakayenijengea nyumba; nami nitahakikisha kwamba ufalme wake unadumu milele. Mimi nitakuwa baba yake, naye atakuwa mwana wangu. Sitaacha kumutendea mema kama vile nilivyoacha kumutendea Saulo aliyekutangulia. Lakini nitamwimarisha katika nyumba yangu na katika ufalme wangu milele, na kiti chake cha kifalme kitakuwa imara siku zote.” Natani akamwelezea Daudi mambo hayo yote kulingana na maono hayo. Kisha mufalme Daudi akaingia ndani ya hema na kuikaa mbele ya Yawe, halafu akaomba: “Mimi ni nani, ee Yawe Mungu, na nyumba yangu ni nini hata unitukuze hivi? Tena jambo hili lilikuwa dogo mbele ya macho yako, ee Mungu. Zaidi ya hayo, umenitolea ahadi juu ya vizazi vyangu vinavyokuja, ee Yawe Mungu! Nikuambie nini zaidi, mimi Daudi mutumishi wako, kwa kunitukuza vile? Wewe unanijua mimi mutumishi wako. Ee Yawe, kwa ajili ya mutumishi wako na kwa kufuatana na moyo wako mwenyewe, umeyatenda hayo makubwa yote, kusudi hayo matendo makubwa yote yajulikane. Hakuna mwingine kama wewe, ee Yawe, na yote tunayosikia yanahakikisha kwamba hakuna Mungu mwingine lakini wewe tu. Tena ni watu gani katika dunia ambao wanaweza kulinganishwa na watu wako Waisraeli? Hao ndio watu peke yao Mungu wao alikwenda kuwakomboa kusudi wakuwe watu wake. Ukajipatia sifa kwa kutenda mambo makubwa na ya ajabu pale ulipofukuza mataifa mbele ya watu wako ambao uliwakomboa kutoka Misri. Hata ukajifanyia watu wako Waisraeli kuwa watu wako milele; nawe ee Yawe, umekuwa Mungu wao. “Basi sasa, ewe Yawe, uimarishe milele neno lako ulilosema juu yangu mimi mutumishi wako na juu ya jamaa yangu. Nalo jina lako litatukuzwa milele, nao watu watasema: ‘Yawe wa majeshi, Mungu wa Israeli, ndiye Mungu juu ya Israeli!’ Na jamaa yangu, mimi Daudi mutumishi wako, itaimarishwa mbele yako. Maana, ee Mungu wangu, nimepata bidii ya kukuomba kwa sababu umenifunulia ukisema kwamba utanipa wazao. Sasa ee Yawe, wewe ndiwe Mungu, umeniahidi mimi mutumishi wako jambo hili jema. Kwa hiyo ninakuomba ubariki wazao wangu, mimi mutumishi wako, kusudi wadumu milele mbele yako; maana unapobariki, baraka zako zinadumu milele.” Nyuma ya hayo, mufalme Daudi aliwashinda na kuwanyenyekeza Wafilistini. Akakamata muji wa Gati pamoja na vijiji vyake vilivyokuwa vya Wafilistini. Akawashinda Wamoabu vilevile, wakakuwa watumishi wake na wakakuwa wanalipa kodi. Daudi akamushinda vilevile Hadadezeri mufalme wa Zoba, inchi iliyokuwa karibu na Hamati, alifanya hivyo wakati alipokuwa akienda kujisimamishia nguzo ya ukumbusho kwenye sehemu za muto Furati. Daudi akanyanganya magari ya vita elfu moja, waaskari wapanda-farasi elfu saba na wa miguu elfu makumi mbili. Kisha Daudi akakata mishipa ya miguu ya nyuma ya farasi wote wa magari, lakini akaacha mia moja. Nao Waaramu wa Damasiki, walipokwenda kumusaidia Hadadezeri mufalme wa Zoba, Daudi akawashambulia na kuwaua watu elfu makumi mbili na mbili. Halafu Daudi akaweka kambi za waaskari katika muji wa Damasiki wa Aramu. Basi Waaramu wakakuwa watumishi wake, na wakakuwa wanalipa kodi. Yawe akamupa Daudi ushindi kokote alikokwenda. Daudi alitwaa ngao za zahabu ambazo waaskari wa Hadadezeri walizobeba, na kuzipeleka Yerusalema. Daudi alichukua vilevile shaba nyingi sana kutoka muji wa Tibuhati na muji wa Kuni iliyokuwa miji ya Hadadezeri. Solomono alitumia shaba hiyo kwa kutengeneza nguzo na vyombo vya shaba. Wakati Toi, mufalme wa Hamati aliposikia kwamba Daudi ameshinda waaskari wote wa Hadadezeri mufalme wa Zoba, akatuma mwana wake Hadoramu kwa mufalme Daudi, kumupelekea salamu na shukrani kwa sababu alikuwa amepigana na Hadadezeri na kumushinda. Maana Hadadezeri alipigana na Toi mara nyingi. Hadoramu alimupelekea Daudi zawadi za vyombo vya feza, zahabu na shaba. Zawadi zile, mufalme Daudi alizitakasa kwa ajili ya Yawe pamoja na feza na zahabu aliyonyanganya kwa mataifa yote, kutoka kwa: Waedomu, Wamoabu, Waamoni, Wafilistini na Waamaleki. Abisai mwana wa Zeruya, akaua Waedomu elfu kumi na nane katika Bonde la Chumvi. Basi akaweka kambi za waaskari kule Edomu. Nao Waedomu wote wakakuwa watumishi wa Daudi. Yawe alimupa Daudi ushindi kokote alikokwenda. Halafu Daudi akatawala juu ya Israeli yote. Aliimarisha haki na sheria ya Mungu kwa watu wote. Yoabu mwana wa Zeruya alikuwa jemadari wa makundi ya waaskari; Yehosafati mwana wa Ahiludi alikuwa mwandishi wa habari za kifalme; Zadoki mwana wa Ahitubu na Ahimeleki mwana wa Abiatari walikuwa makuhani; Sausa alikuwa katibu; na Benaya mwana wa Yehoyada alikuwa mwangalizi wa waaskari walinzi wa Daudi; wana wa Daudi walikuwa na vyeo vikubwa katika utawala wake. Nyuma ya hayo, Nahasi mufalme wa Waamoni akakufa, na mwana wake Hanuni akatawala kwa pahali pake. Basi, Daudi akasema: “Nitamutendea mema Hanuni mwana wa Nahasi, maana baba yake alinitendea mema vilevile.” Halafu Daudi akatuma wajumbe na kumupelekea salamu za pole kwa ajili ya kifo cha baba yake. Nao wakaenda kwa Hanuni kwa kumufariji, kule katika inchi ya Waamoni. Lakini viongozi wa Waamoni wakamwambia mufalme: “Unazani ni kwa sababu ya heshima ya baba yako ndiyo maana Daudi anatuma wajumbe hawa wakuje kukufariji? Watu hawa ni wapelelezi waliotumwa kuja kuichunguza inchi kwa kuiangamiza na kuipeleleza.” Basi Hanuni aliwatwaa wajumbe wale wa Daudi, akawanyoa ndevu na kupasua nguo zao katikati mpaka kwenye matako, kisha akawaacha waende zao, nao wakaondoka na kurudi kwao. Daudi alipopashwa habari jinsi wajumbe wake walivyotendewa, akatuma watu kwa kuwapokea maana wale wajumbe waliona haya sana. Naye mufalme akawaambia: “Mukae katika muji wa Yeriko, mpaka mutakapoota ndevu, kisha murudi.” Waamoni walipoona wamejifanya wachukizwe na Daudi, Hanuni na wale Waamoni wakatuma watu wapeleke kilo elfu makumi tatu za feza kwa kulipa magari ya vita na waaskari wapanda-farasi kutoka Mesopotamia, Aramaka na Zoba. Walikopesha magari elfu makumi tatu na mawili, na mufalme wa Maka na waaskari wake akakuja na kupiga kambi karibu na Medeba. Waamoni walikusanyika toka kwenye miji yao yote, wakajiweka tayari kwa vita. Naye Daudi aliposikia habari hizo akatuma Yoabu na kundi lote la waaskari mashujaa. Waamoni wakatoka na kujipanga kwenye mulango wa muji, wakati wale wafalme waliokuja walikuwa peke yao kwenye mbuga. Yoabu alipoona kwamba vita ni kali juu yake, mbele na nyuma, akachagua waaskari hodari zaidi kati ya Waisraeli, akawapanga mbele ya Waaramu. Wale waaskari wengine waliobaki, akawaweka chini ya uongozi wa ndugu yake Abisai, naye akawapanga waangaliane na Waamoni. Yoabu akamwambia Abisai: “Ikiwa Waaramu wananizidi nguvu, utanisaidia; lakini kama Waamoni wanakuzidi nguvu, nitakuja kukusaidia. Basi ukuwe hodari! Tupigane kama wanaume kwa ajili ya watu wetu, na kwa ajili ya miji ya Mungu wetu; na Yawe atutendee sawa na mapenzi yake.” Basi, Yoabu na watu wake walisonga mbele kwa kupigana na Waaramu, nao Waaramu wakakimbia. Waamoni walipoona Waaramu wamekimbia, nao walimukimbia Abisai, ndugu ya Yoabu, wakaingia katika muji. Halafu Yoabu akarudi Yerusalema. Lakini Waaramu walipoona kwamba wameshindwa na Waisraeli, wakatuma wajumbe waende kuwaleta Waaramu wengine waliokuwa ngambo ya muto Furati wakiongozwa na Sofaki, jemadari wa jeshi la Hadadezeri. Daudi alipopata habari, akakusanya pamoja Waisraeli wote, akavuka muto Yordani, akawaendea, akapanga vikundi vyake mbele yao. Daudi alipopanga vita juu ya Wasuria, basi nao wakapigana naye. Lakini Waaramu wakakimbia mbele ya Waisraeli. Daudi akawaua Waaramu wanaoendesha magari elfu saba na waaskari wa miguu elfu makumi ine. Vilevile akamwua Sofaki, jemadari wa jeshi lao. Kisha watumishi wa Hadadezeri walipoona kwamba wameshindwa na Waisraeli, wakafanya mapatano ya amani na Daudi nao wakakuwa watumishi wa Daudi. Halafu Waaramu hawakukubali kuwasaidia Waamoni tena. Ilipokuwa wakati wa kipwa, wakati ambapo wafalme wanaenda kwa vita, Yoabu akaongoza jeshi na kuharibu inchi ya Waamoni, akaenda vilevile na kuzunguka muji wa Raba kwa vita. Lakini Daudi alibaki kule Yerusalema. Naye Yoabu akashambulia muji wa Raba na kuuteka. Kisha Daudi akatwaa taji ya mufalme wao kutoka juu ya kichwa chake, naye akagundua kwamba taji hiyo ilikuwa na uzito wa kilo makumi tatu na tano za zahabu na ndani yake mulikuwa jiwe la bei kali. Daudi akavikwa taji hiyo juu ya kichwa chake. Vilevile alinyanganya vitu vingi sana kutoka katika muji ule. Halafu akakamata watu wa muji ule, nao wakafanya kazi wakitumia misumeno, sururu za chuma na mashoka ya chuma. Ni vile ndivyo alivyoitendea miji yote ya Waamoni. Kisha Daudi na watu wote wakarudi Yerusalema. Nyuma ya hayo, kukatokea vita na Wafilistini kule Gezeri. Sibekayi wa muji wa Husati akamwua Sipayi aliyekuwa mumoja kati ya wazao wa majitu; hivyo Wafilistini wakashindwa. Kukatokea tena vita na Wafilistini. Naye Elihanani mwana wa Yairi akamwua Lami ndugu ya Goliati wa muji wa Gati ambaye mupini wa mukuki wake ulikuwa kama muti wa mufumaji wa nguo. Nyuma kukatokea tena vita kule Gati ambako kulikuwa mutu mumoja aliyekuwa murefu sana, na vidole sita katika kila mukono, na vidole sita katika kila muguu, kwa jumla vidole makumi mbili na vine. Yeye vilevile alikuwa wa uzao wa majitu. Naye alipowatukana Waisraeli, Yonatani mwana wa Simea, ndugu ya Daudi, akamwua. Hao walikuwa wazao wa majitu kule Gati, nao wakauawa na Daudi pamoja na watumishi wake. Shetani akaenda kinyume cha Waisraeli, akamushawishi Daudi kuwahesabu watu. Halafu, Daudi akamwambia Yoabu na wale majemadari wengine: “Mwende muwahesabu Waisraeli, kutokea Beri-Seba mpaka Dani. Muniletee habari kusudi nijue hesabu yao.” Lakini Yoabu akasema: “Yawe aongeze Waisraeli mara mia kuliko jinsi wanavyokuwa sasa! Bwana wangu mufalme, hawa wote si watumishi wako? Kwa nini basi unataka kufanya jambo ambalo litawatia Waisraeli katika kosa?” Lakini amri ya mufalme ilikuwa na nguvu zaidi mbele ya Yoabu. Halafu, Yoabu akaenda katika inchi ya Israeli yote, kisha akarudia Yerusalema. Yoabu akamupelekea mufalme Daudi hesabu ya watu: katika inchi yote wa Israeli kulikuwa wanaume milioni moja na elfu mia moja, wenye ujuzi wa kutumia mapanga, na katika inchi ya Yuda kulikuwa watu elfu mia ine na makumi saba wenye kutumia mapanga. Lakini Yoabu hakuwahesabu Walawi na watu wa kabila la Benjamina, kwa sababu alichukizwa sana na amri ya mufalme. Mungu hakupendezwa na jambo lile kwa hiyo akaazibu Waisraeli. Daudi akamwambia Mungu: “Nimetenda zambi kubwa kwa tendo hili nililofanya! Lakini ninakuomba unisamehe mimi mutumishi wako, maana nimefanya jambo la kipumbafu kabisa.” Basi, Yawe akasema na Gadi, mutabiri wa Daudi, akamwambia: “Kwenda kumwambia Daudi hivi: ‘Yawe anasema hivi: Ninakupa mambo matatu, nawe ujichagulie moja kati yao, nami nitakutendea vile.’ ” Halafu Gadi akamwendea Daudi na kumwambia: “Yawe anasema hivi: ‘Ujichagulie jambo moja unalotaka kati ya haya: njaa ya miaka mitatu; au miezi mitatu ya maangamizi kutokana na waadui zako ambapo upanga wa waadui zako utakushinda; au siku tatu ambazo Yawe atawashambulia kwa upanga wake, awaletee ugonjwa mukali katika inchi, na malaika wake apite kuwaangamiza katika inchi nzima ya Israeli. Sasa amua. Ni jibu gani nitakalomupa yeye aliyenituma.’ ” Daudi akamujibu Gadi: “Nimeingia katika mashaka makubwa! Lakini afazali niazibiwe na Yawe maana yeye ana huruma sana. Lakini nisianguke katika mukono wa mwanadamu.” Basi, Yawe akawaletea Waisraeli ugonjwa mukali, ambao ulisababisa vifo vya Waisraeli elfu makumi saba. Halafu Mungu akatuma malaika aende kuharibu Yerusalema. Lakini mbele hajafanya vile, Yawe akageuza nia yake na kumwambia malaika yule aliyetimiza maangamizi: “Basi, inatosha!” Malaika alikuwa amesimama karibu na uwanja wa kupepetea ngano wa Ornani wa kabila ya Yebusi. Daudi akainua macho yake, akamwona yule malaika wa Yawe akisimama kati ya mbingu na dunia, naye akiinua upanga wake juu ya Yerusalema tayari kuangamiza. Halafu Daudi na wazee wote walikuwa wakivaa nguo ya gunia, wakaanguka uso mpaka chini. Daudi akamwambia Mungu: “Si mimi ndiye niliyetoa amri watu wahesabiwe? Ni mimi niliyetenda zambi na kufanya uovu. Lakini kondoo hawa wamefanya nini? Ninakusihi sana, ee Yawe, Mungu wangu, mukono wako ukuwe juu yangu na juu ya jamaa ya baba yangu, lakini ugonjwa huu mukali usiwapate watu wako.” Halafu malaika wa Yawe akamwamuru Gadi amwambie Daudi aende kumujengea Yawe mazabahu, katika kiwanja cha kupepetea ngano cha Ornani wa kabila ya Yebusi. Daudi akatii amri ya Yawe, akapanda juu kufuatana na neno Gadi alilosema kwa jina la Yawe. Ornani alipogeuka na kumwona yule malaika, halafu yeye na wana wake wane waliokuwa pamoja naye wakajificha. Naye Ornani alikuwa akipepeta ngano. Daudi alipomwendea Ornani akaangalia na kumwona Daudi. Basi Ornani akatoka kwenye uwanja wa kupepetea na kwenda mbele, kisha akainama mbele yake uso mpaka chini. Daudi akamwambia Ornani: “Unipe nafasi ya uwanja wako wa kupepetea ngano kusudi nimujengee Yawe mazabahu juu yake, kusudi ugonjwa mukali upate kuzuiliwa katika watu. Uniuzishie kwa bei yake kamili.” Naye Ornani akamwambia Daudi: “Utwae kiwanja hiki, bwana wangu mufalme, na ukitumie vile unavyopenda mwenyewe. Angalia, ninawatoa ngombe dume kwa ajili ya sadaka za kuteketezwa kwa moto, na vifaa vya kupepetea kwa kuni, pamoja na ngano ikuwe sadaka ya unga. Vyote hivyo ninakupa.” Lakini mufalme Daudi alimwambia Ornani: “Hapana; nitavinunua kwa bei yake kamili. Sitamutwalia Yawe kitu chako au kumutolea sadaka za kuteketezwa kwa moto ambazo sikununua.” Hivyo, Daudi akamulipa Ornani kwa bei ya vikoroti mia sita kamili vya zahabu kwa kulipia uwanja ule. Kisha Daudi akamujengea Yawe mazabahu pahali pale na kumutolea sadaka za kuteketezwa kwa moto na sadaka za amani. Akamwomba Yawe, naye akakubali maombi yake kwa kuleta moto kutoka mbinguni na kuteketeza sadaka kwenye mazabahu. Halafu, Yawe akamwamuru malaika, naye akaweka upanga wake ndani ya mufuko wake. Wakati ule, Daudi alipoona kwamba Yawe amekubali maombi yake kwenye uwanja wa kupepetea ngano wa Ornani, Muyebusi, akatoa sadaka palepale. Hema la Yawe ambalo lilitengenezwa na Musa katika jangwa, na mazabahu ya sadaka ya kuteketezwa, wakati ule vilikuwa bado pale pahali pa kuabudia kule Gibeoni. Lakini Daudi hakuweza kwenda kule kumwomba Mungu shauri kwa sababu alikuwa anaogopa upanga wa malaika wa Yawe. Basi Daudi akasema: “Hapa ndipo pahali ambapo nyumba ya Yawe itakuwa, na hii ndiyo mazabahu ambapo watu wa Israeli watatolea sadaka ya kuteketezwa kwa moto.” Daudi akatoa amri kwamba wageni wote waliokuwa katika inchi ya Israeli wakusanyike, naye akawapangia kazi. Akaweka wamoja wachonge vizuri mawe ya kujenga nyumba ya Mungu. Daudi akaweka vilevile akiba tele ya chuma cha kutengeneza misumari na vifungio vya milango ya nyumba, na akiba tele ya shaba isiyopimika. Mbao za mierezi ambazo Daudi aliletewa na Wasidoni na Watiro zilikuwa hazihesabiki. Daudi akajisemesha: “Nyumba ambayo mwana wangu Solomono atakayomujengea Yawe itakuwa nzuri sana, ya kusifiwa na tukufu katika dunia yote. Lakini kwa vile yeye bado angali kijana na bado hana maarifa mengi, afazali nimufanyie matayarisho.” Hivyo basi, Daudi akaweka akiba kubwa sana ya vitu vya kujenga mbele ya kufa kwake. Halafu Daudi akamwita mwana wake Solomono, akamwagiza amujengee Yawe, Mungu wa Israeli, nyumba. Daudi akamwambia Solomono: “Mwana wangu, nilikusudia ndani ya moyo wangu kumujengea Yawe, Mungu wangu, nyumba kwa kumutukuza. Lakini neno la Yawe lilinifikia kusema hivi: ‘Wewe umemwanga damu nyingi na kupigana vita kubwa. Kwa sababu ya damu nyingi ambayo umemwanga mbele yangu hapa katika dunia, hautanijengea nyumba. Hata hivyo, utapata mwana ambaye atatawala kwa amani kwa sababu nitamupa amani na waadui zake wote wa jirani. Jina lake litakuwa Solomono, kwa maana katika siku za utawala wake, atailetea inchi ya Israeli amani na utulivu. Hivyo, yeye ndiye atakayenijengea nyumba. Atakuwa mwana wangu nami nitakuwa baba yake, na wazao wake watatawala Israeli milele.’ “Sasa, mwana wangu, Yawe, Mungu wako, akuwe pamoja nawe kusudi uweze kumujengea nyumba kama vile alivyosema. Yawe akupe hekima na akili kusudi atakapokupa uongozi juu ya Israeli, ushike sheria za Yawe, Mungu wako. Ukiwa mwangalifu, na ukitii masharti na maagizo ambayo Yawe alimwagiza Musa juu ya Israeli, utastawi. Ujipe moyo, ukuwe imara. Usiogope wala usifazaike. Kwa juhudi kubwa, nimeiwekea akiba nyumba ya Yawe zaidi ya toni elfu tatu za zahabu, zaidi ya toni elfu moja za feza pamoja na shaba na chuma visivyoweza kupimwa maana ni vingi sana. Nimetayarisha mbao na mawe. Lakini utaweza kuongeza. Uko na watumishi wengi: kuna wachongaji wa mawe, wajengaji, waseremala na wafundi wa kila aina wenye ujuzi mwingi wa kufua zahabu, feza, shaba na chuma. Basi sasa, anza kazi! Yawe akuwe pamoja nawe!” Zaidi ya hayo, Daudi akawaamuru viongozi wote wa Waisraeli wamusaidie mwana wake Solomono, akisema: “Yawe, Mungu wenu hayuko pamoja nanyi? Hajawapa amani katika pande zote? Yeye aliwatia wakaaji wa inchi hii katika mikono yangu na sasa wako chini ya Yawe na watu wake. Sasa, mumutumikie Yawe, Mungu wenu, kwa nia na moyo wote. Basi mujitayarishe kumujengea Yawe pahali patakatifu kusudi Sanduku la Agano la Yawe pamoja na vyombo vyote vitakatifu vinavyotumiwa katika ibada, viwekwe ndani ya nyumba iliyojengwa kwa ajili ya Yawe.” Daudi alipokuwa muzee wa miaka mingi, akamuweka Solomono mwana wake kuwa mufalme wa Israeli. Mufalme Daudi akawakusanya wakubwa wote wa Israeli, makuhani na Walawi. Walawi wote wanaume wenye umri wa miaka makumi tatu na zaidi, wakahesabiwa. Jumla yao ilikuwa elfu makumi tatu na nane. Halafu, Daudi akawagawanya: elfu makumi mbili na nane kati yao wakuwe wasimamizi wa kazi ya nyumba ya Yawe, elfu sita wakuwe wakubwa na waamuzi, elfu ine wakuwe walinzi wa milango, na elfu ine wakuwe waimbaji, wakimusifu Yawe kwa ala za muziki mufalme alizotengeneza mwenyewe kwa ajili ya kazi hiyo. Daudi akawagawanya Walawi katika makundi matatu kulingana na ukoo za kabila la Lawi: ukoo wa Gersoni, ukoo wa Kohati na ukoo wa Merari. Wana wa Gersoni walikuwa: Ladani na Simei. Wana wa Ladani walikuwa watatu: Yehieli mukubwa wao, Zetamu na Yoeli. Wana wa Simei walikuwa watatu: Selomoti, Hazieli na Harani. Hawa walikuwa viongozi wa ukoo wa Ladani. Wana wengine wane wa Simei walikuwa: Yahati, Zina, Yeusi na Beria. Yahati ndiye aliyekuwa mukubwa wao, akifuatwa na Zina. Lakini Yeusi na Beria, kwa vile hawakukuwa na wana wengi, walihesabiwa kama vile ukoo mumoja. Wana wa Kohati walikuwa wane: Amuramu, Isari, Hebroni na Usieli. Wana wa Amuramu walikuwa: Haruni na Musa. Haruni alichaguliwa kwa kazi inayoelekea vitu vitakatifu kabisa, hata wazao wake siku zote wafukizie ubani mbele ya Yawe, wakimutumikia na kuwabariki watu katika jina la Yawe milele. Lakini wana wa Musa, mutu wa Mungu wanatajwa katika kabila la Lawi. Wana wa Musa walikuwa: Gersoni na Eliezeri. Mukubwa kati ya wana wa Gersoni alikuwa: Sebueli. Mwana wa pekee wa Eliezeri alikuwa: Rehabia. Rehabia alikuwa na wana wengi sana. Mwana wa Isari alikuwa: Selomiti, kiongozi wa kabila zima. Wana wa Hebroni walikuwa: Yeria, mukubwa wao; Amaria, wa pili; Yahazieli, wa tatu; na Yekameamu, wa ine. Wana wa Uzieli walikuwa: Mika mukubwa wao, na Isia wa pili. Wana wa Merari walikuwa: Mali na Musi. Wana wa Mali walikuwa: Eleazari na Kisi. Eleazari alikufa bila mwana, lakini wabinti tu. Wabinti wale wakaolewa na binamu zao, wana wa Kisi. Wana wa Musi walikuwa watatu: Mali, Ederi na Yeremoti. Hao ndio wana wa Lawi kulingana na ukoo zao. Kila mumoja wao aliyetimiza umri wa miaka makumi mbili na zaidi, aliandikishwa kwa jina, na alishiriki katika kazi ya kujenga nyumba ya Yawe. Daudi akasema: “Yawe, Mungu wa Israeli, amewapa watu wake amani, naye ataishi Yerusalema kwa milele. Kwa hiyo, Walawi hawatahitaji tena kubeba hema takatifu au vyombo vyake vya ibada.” Kulingana na maagizo ya mwisho Daudi aliyotoa, Walawi wote waliofikia umri wa miaka makumi mbili waliandikishwa. Kazi yao ilikuwa ni kuwasaidia makuhani wa ukoo wa Haruni katika kazi ya kujenga nyumba ya Yawe, kutunza viwanja na vyumba, kusafisha vyombo vitakatifu vyote na kufanya kazi zinazoelekea kujenga nyumba ya Yawe. Pamoja na hayo, walisaidia katika kazi kutayarisha mikate mitakatifu, unga safi na sadaka ya vyakula, maandazi yasiyotiwa chachu, sadaka ya mikate iliyokaangwa, sadaka ya mikate iliyochanganywa na mafuta, na sadaka katika kazi ya upimaji wa wingi wa sadaka na ukubwa wake. Walisimama kwa kumushukuru na kumusifu Yawe kila siku asubui na magaribi, na wakati wa siku za Sabato, mwandamo wa mwezi na sikukuu zingine, pale sadaka za kuteketezwa kwa moto zilipotolewa kwa Yawe. Sheria ziliwekwa kuelekea hesabu ya Walawi walioagizwa kufanya kazi zile siku zote mbele ya Yawe. Kwa hiyo, ilikuwa ni kazi yao kutunza hema la kusanyiko na Pahali Patakatifu, na kuwasaidia wandugu zao makuhani, wazao wa Haruni, kwenye ibada katika nyumba ya Yawe. Hayo ndiyo makundi ya wana wa Haruni. Haruni alikuwa na wana wane: Nadabu, Abihu, Eleazari na Itamari. Nadabu na Abihu walikufa mbele ya baba yao, wala hawakukuwa na watoto; kwa hiyo wandugu zao Eleazari na Itamari wakakuwa makuhani. Mufalme Daudi akawapanga wana wa Haruni katika makundi kufuatana na kazi zao. Alisaidiwa kufanya hivyo na Zadoki, wa uzao wa Eleazari, na Ahimeleki, wa uzao wa Itamari. Kwa vile ambavyo kulipatikana viongozi wanaume wengi zaidi kati ya wazao wa Itamari, wakawagawanya wana wa Eleazari chini ya viongozi kumi na sita, na wana wa Itamari chini ya viongozi wanane. Waligawanywa kwa kupiga kura maana kulikuwa wakubwa wa Pahali Patakatifu na viongozi wa Mungu kati ya ukoo zote mbili; ukoo wa Eleazari na ukoo wa Itamari. Naye Semaya mwana wa Nataneli, mwandishi, aliyekuwa Mulawi, akawaandika mbele ya mufalme Daudi, wakubwa wake, kuhani Zadoki, Ahimeleki mwana wa Abiatari na viongozi wa jamaa za makuhani na za Walawi; ukoo wa Eleazari ukatwaliwa kwa kupiga kura mbili na ukoo wa Itamari kwa kupiga kura moja. Hawa waliandikishwa kulingana na kazi zao kuingia katika nyumba ya Yawe kutumika kwa kadiri ya utaratibu waliowekewa na babu yao Haruni, kama vile alivyoamuriwa na Yawe, Mungu wa Israeli. Vilevile hao wote walipiga kura kufuatana na ukoo wa kila mukubwa na mudogo wake, kama vile wazao wa Haruni walivyofanya. Walipiga kura mbele ya mufalme Daudi, Zadoki, Ahimeleki na viongozi wa jamaa za makuhani na za Walawi. Mufalme Daudi na viongozi wa Walawi, wakachagua wazao wa Asafu, wa Hemani, na wa Yedutuni, kwa kuongoza katika kazi ya kutabiri kwa kutumia vinubi, na vinanda na matoazi. Haya ndiyo majina ya wale waliochaguliwa kwa kuongoza ibada, pamoja na aina ya kazi iliyofanywa na kila kikundi: Wana wa Asafu: Zakuri, Yosefu, Netania na Asarela. Hao walikuwa chini ya uongozi wa Asafu aliyetabiri wakati wote chini ya uongozi wa mufalme. Wana wa Yedutuni: Gedalia, Seri, Yesaya, Simei, Hasabia na Matitia. Wao walikuwa chini ya uongozi wa baba yao; na walitabiri kwa kutumia vinubi, na wakimushukuru na kumutukuza Yawe. Wana wa Hemani: Bukia, Matania, Usieli, Sebueli, Yeremoti, Hanania, Hanani, Eliyata, Gidalti, Romamuti-Ezeri, Yosibekasa, Maloti, Hotiri na Mahasioti. Mungu alimupatia Hemani aliyekuwa akitabiria mufalme, wana hawa kumi na wane, na wabinti watatu, kama vile alivyoahidi kwa kumutukuza. Wana wake wote walipiga muziki kwa matoazi, vinanda na vinubi, kwenye ibada katika nyumba ya Yawe wakiwa chini ya uongozi wa baba yao. Asafu, Yedutuni na Hemani walikuwa chini ya uongozi wa mufalme. Hesabu yao pamoja na wale wandugu zao Walawi waliofundishwa kumwimbia Yawe, wote waliokuwa wafundi, ilikuwa mia mbili na makumi nane na wanane. Haya ndiyo makundi ya Walawi waliofanya kazi za ulinzi. Kutoka katika ukoo wa Kora, kulikuwa Meselemia mwana wa Kora wa jamaa ya Asafu. Meselemia alikuwa na wana saba: Zekaria muzaliwa wake wa kwanza, Yediaeli wa pili, Zebadia wa tatu, Yatinieli wa ine, Elamu wa tano, Yohanani wa sita na Eliehoenai wa saba. Vilevile kulikuwa Obedi-Edomu, ambaye Mungu alimubariki kwa kumupa wana wanane: Semaya muzaliwa wake wa kwanza, Yehozabadi wa pili, Yoa wa tatu, Sakari wa ine, Netaneli wa tano, Amieli wa sita, Isakari wa saba na Peuletayi wa nane. Mwana wake Semaya alizaa wana. Walikuwa na mamlaka juu ya jamaa ya baba yao kwa sababu walikuwa wanaume wenye uwezo mukubwa. Wana wa Semaya walikuwa: Otini, Refaeli, Obedi, Elizabadi, wandugu zake walikuwa mashujaa, Elihu na Semakia. Hao wote walikuwa wana wa Obedi-Edomu; wao na wana wao na wandugu zao, walikuwa watu hodari katika utumishi wao. Wazao wote wa Obedi-Edomu walikuwa makumi sita na wawili. Naye Meselemia alikuwa na wana na wandugu zake; watu wenye uwezo kumi na wane. Hosa mumoja kati ya wana wa Merari alikuwa na wana wane: Simuri (aliyefanywa kiongozi na baba yake hata ingawa hakukuwa muzaliwa wa kwanza), Hilkia wa pili, Tebalia wa tatu na Zekaria wa ine. Wana wote wa Hosa pamoja na wandugu zao walikuwa kumi na watatu. Hao walinzi wa milango waligawanyika katika makundi kulingana na jamaa zao, nao vilevile walipangiwa kazi kwenye nyumba ya Yawe kama wale Walawi wengine. Kila jamaa, bila kujali wingi ilipiga kura kwa kuchagua mulango watakaosimamia. Kura ya kuchagua wa kulinda mulango wa upande wa mashariki ikamwangukia Selemia. Wakapiga kura vilevile kwa ajili ya mwana wake Zekaria, aliyekuwa mushauri mwenye hekima, ikamwangukia kura ya mulango wa upande wa kaskazini. Obedi-Edomu akaangukiwa na kura ya mulango wa upande wa kusini. Wana wake wakaangukiwa na kura ya gala. Supimu na Hosa wakaangukiwa na kura ya kulinda mulango wa upande wa magaribi kwenye mulango wa Saleketi kwenye barabara ya juu. Ulinzi ulifanywa kwa zamu. Kila siku upande wa mashariki kulikuwa walinzi sita, kaskazini wane, na kusini wane, vilevile kwenye gala kuliwekwa walinzi wawili wawili; na kwenye banda zuri lililokuwa upande wa magaribi, kulikuwa walinzi wane katika barabara na wawili kwenye banda lenyewe. Haya ndiyo makundi ya walinzi kati ya ukoo wa Kora na ya wazao wa Merari waliofanya kazi ya ulinzi wa milango. Kati ya Walawi, Ahia alielekea uangalizi wa hazina ya nyumba ya Mungu, na hazina na vitu vitakatifu. Ladani, mumoja wa ukoo wa Gersoni, alikuwa babu wa jamaa nyingi, kati yao kukiwa jamaa ya mwana wake Yehieli. Wana wengine wawili wa Ladani, Zetamu na Yoeli, walikuwa wachungaji wa hazina ya nyumba ya Yawe. Vilevile kazi ziligawanywa kwa watu wa ukoo za Waamuramu, Waisihari, Wahebroni na Wauzieli. Sebueli mwana wa Gersoni, mujukuu wa Musa, alikuwa musimamizi mukubwa wa hazina zile. Na ndugu yake, alikuwa Eliezeri, aliyekuwa baba ya Rehabia. Rehabia alikuwa baba ya Yesaya, aliyemuzaa Yoramu, Yoramu alizaa Zikiri, Zikiri alizaa Selomoti. Selomoti na wandugu zake, ndio waliokuwa waangalizi wa hazina zote za vitu vitakatifu ambavyo mufalme Daudi alitoa kwa Mungu, viongozi wa jamaa, majemadari wa maelfu na mamia na majemadari wa jeshi. Walichunga sehemu ya vitu walivyonyanganya katika vita kwa ajili ya kutengeneza nyumba ya Yawe. Vilevile vitu vyote vilivyotolewa kwa Mungu na nabii Samweli na Saulo mwana wa Kisi, na Abeneri, na Yoabu mwana wa Zeruya, vilikuwa chini ya uangalizi wa Selomiti na wandugu zake. Kati ya watu wa ukoo wa Isiari, Kenania na wana wake walipewa kazi za utawala kama kusimamia watu na waamuzi, kwa ajili ya Waisraeli. Kati ya watu wa ukoo wa Hebroni, Hasabia na wandugu zake elfu moja na mia saba, wote watu mashujaa walipewa kazi ya kusimamia sehemu za inchi ya Israeli zilizokuwa upande wa magaribi wa muto Yordani. Walisimamia kazi yote ya Yawe na kazi za mufalme Daudi. Kati ya watu wa ukoo wa Hebroni, Yeria alikuwa kiongozi wa ukoo na jamaa zote, na katika mwaka wa makumi ine wa utawala wa mufalme Daudi, uchunguzi ulifanywa na wanaume wenye uwezo mukubwa wakapatikana kule Yezeri katika jimbo la Gileadi. Mufalme Daudi alimuchagua Yeriya na wandugu zake elfu mbili na mia saba, mashujaa na viongozi wa ukoo, kwa kusimamia mambo yote yaliyoelekea Mungu na mufalme Daudi katika sehemu za watu wa ukoo wa Rubeni, Gadi na nusu ya kabila la Manase, zilizokuwa upande wa mashariki wa muto Yordani. Haya ndiyo majina ya wana wa Israeli waliokuwa viongozi wa jamaa, na majemadari wa maelfu na mamia na wakubwa wao waliomutumikia mufalme Daudi juu ya zamu za kuingia na kutoka. Kila mwezi katika mwaka, kundi tofauti la watu elfu makumi mbili na ine walishika zamu ya kufanya kazi. Mufalme Daudi hakuwahesabu wale waliokuwa chini ya umri wa miaka makumi mbili kwa maana Yawe aliahidi kuwaongeza Waisraeli kuwa wengi kama nyota za mbinguni. Yoabu mwana wa Zeruya alianza kuwahesabu lakini hakumaliza; tena kasirani iliwapata Waisraeli kwa ajili ya tendo hili, nayo hesabu haikuingizwa katika kitabu cha habari za mufalme Daudi. Yonatani, mujomba wa mufalme Daudi, alikuwa mushauri na mutu mwenye ufahamu na mwandishi. Yehieli mwana wa Hakemoni aliwafundisha wana wa mufalme. Mufalme Daudi akakusanya kule Yerusalema wakubwa wote wa Waisraeli: wa makabila, majemadari na vikundi waliomutumikia mufalme, wakubwa wa maelfu na mamia, wasimamizi wa mali yote, ya ngombe wote wa mufalme na wana wake pamoja na wakubwa wa nyumba ya kifalme, mashujaa na waaskari wenye heshima. Halafu mufalme Daudi akasimama na kusema: “Enyi wandugu zangu na watu wangu, munisikilize. Nilikusudia ndani ya moyo wangu kujenga nyumba kwa ajili ya Sanduku la Agano la Yawe, kiti cha kuwekea miguu ya Mungu wetu; na nilifanya matayarisho ya kujenga. Lakini Mungu alinikataza, kwa sababu mimi ni mutu wa vita na nimekwisha mwanga damu nyingi. Lakini Yawe, Mungu wa Israeli, alinichagua mimi kati ya jamaa ya baba yangu kuwa mufalme wa Israeli kwa milele. Alichagua kabila la Yuda kusudi liongozeke; na kutokana na kabila lile, alichagua jamaa ya baba yangu, na kati ya wana wa baba yangu, alipendezwa nami na kuniweka nikuwe mufalme wa Israeli yote. Yawe amenijalia wana wengi, na kati ya hao wote, amemuchagua Solomono mwana wangu, aikae juu ya kiti cha kifalme cha ufalme wa Yawe atawale. “Yawe aliniambia: ‘Mwana wako Solomono ndiye atakayenijengea nyumba na viwanja vyangu, kwa maana nimemuchagua yeye akuwe mwana wangu, nami nitakuwa baba yake.’ Nitaimarisha ufalme wake milele ikiwa ataendelea kushika kwa moyo amri zangu na maagizo yangu kama vile anavyofanya leo. “Basi sasa, mbele ya kusanyiko hili la Waisraeli wote, taifa la watu wa Yawe, na mbele ya Mungu wetu, muangalie na mushike amri zote za Yawe, Mungu wenu, kusudi muendelee kurizi inchi hii nzuri, na kuwarizisha wazao wenu nyuma yenu, hata milele. “Nawe Solomono mwana wangu, umujue Mungu wa baba yako, na umutumikie kwa moyo wako wote na kwa nia nzuri; yeye Yawe anachunguza mioyo na anafahamu mipango na mafikiri ya mwanadamu. Ukimutafuta yeye, utamwona; lakini ukimwacha, atakutupilia mbali milele. Basi fanya angalisho na kukumbuka kwamba Yawe amekuchagua wewe umujengee nyumba ya ibada. Ukuwe hodari na utende hivyo.” Halafu Daudi akamupa Solomono mwana wake mufano wa majengo yote ya hekalu, nyumba zake, hazina zake, gorofi zake, vyumba vyake vya ndani na pahali pa kiti cha rehema. Alimupatia mufano wa yote aliyokusudia ndani ya moyo juu ya viwanja vya nyumba ya Yawe, vyumba vya Mungu na gala za kuwekea vitu vitakatifu. Akamupatia vilevile mufano wa jinsi ya kuwapanga makuhani na Walawi kwa kutimiza kazi zao, kutumikia nyumba ya Yawe na kutunza vyombo vyote vya nyumba ya Yawe. Alimupatia kiasi cha zahabu iliyohitajika kwa kutengeneza vyombo vyote vya zahabu vya utumishi wa kila namna, kiasi cha feza iliyohitajika kwa utumishi wa kila namna, uzito wa vinara vya zahabu na taa zake, uzito wa kila kinara na taa zake kiasi cha feza ya kutengeneza kinara na taa zake kulingana na matumizi ya kila kinara; na kiasi cha zahabu ya kutengeneza meza za zahabu za kuwekea mikate iliyotolewa kwa Mungu, hata kiasi cha feza ya kutengeneza meza za feza; vilevile alitoa maagizo juu ya kiasi cha zahabu safi iliyohitajika kwa kutengeneza makanya, mabeseni na vikombe, vilevile kiasi cha zahabu na feza iliyohitajika kwa kutengeneza mabakuli ya zahabu na ya feza, na kiasi cha zahabu safi ya kutengeneza mazabahu ya kufukizia ubani. Alimupatia vilevile mufano wake wa gari la zahabu la makerubi yaliyotandaza mabawa na kufunika Sanduku la Agano la Yawe. Hayo yote, mufalme Daudi aliyaweka wazi kwa maandiko aliyopewa na Yawe. Kazi yote itendeke kulingana na mufano ule. Kisha, mufalme Daudi akamwambia Solomono mwana wake: “Uwe imara na hodari, ufanye kazi hii. Usiogope wala kuwa na wasiwasi. Yawe Mungu ambaye ni Mungu wangu, yuko pamoja nawe. Hatakuachilia lakini atakuwa nawe mpaka itakapomalizika kazi yote ambayo inayohitajika kufanyiwa kwa nyumba ya Yawe. Makuhani na Walawi wamekwisha kupangiwa kazi watakazofanya katika nyumba ya Mungu. Watumishi wenye ujuzi wa kila aina watakuwa tayari kabisa kukusaidia, na watu wote pamoja na viongozi wao watakuwa chini ya mamlaka yako.” Mufalme Daudi akawaambia wale watu wote waliokusanyika: “Solomono mwana wangu, ambaye peke yake amechaguliwa na Mungu, angali bado mudogo, hana maarifa mengi na kazi hii ni kubwa. Nyumba atakayojenga si ya mwanadamu, lakini ni ya Mungu, Yawe. Basi nimejitia kwa kadiri ya uwezo wangu wote kwa kuwekea nyumba ya Mungu wangu, akiba ya zahabu ya kutengeneza vitu vya zahabu, feza ya kutengeneza vitu vya feza, shaba ya kutengeneza vitu vya shaba, chuma cha kutengeneza vitu vya chuma, na miti ya kutengeneza vitu vya miti. Zaidi ya hayo, nimetayarisha kwa wingi mawe ya rangi na mawe ya kupamba, mawe ya kuchorwa, mawe ya bei kali ya kila namna na marumaru. Tena zaidi ya vyote nilivyotoa kwa ajili ya nyumba takatifu, nina hazina yangu ya pekee ya zahabu na feza, na kwa sababu ninapenda nyumba ya Mungu wangu ninaitoa kwa nyumba ya Mungu wangu; ni toni mia moja za zahabu kutoka Ofiri, toni yapata mia mbili za feza safi ya kuzifunikia kuta za nyumba, na kwa ajili ya kutengeneza vitu vya kila aina vitakavyotengenezwa na wafundi kwa mikono. Nimeweka zahabu kwa ajili ya vyombo vya zahabu, na feza kwa ajili ya vyombo vya feza. Ni nani basi atakayemutolea Yawe kwa mapenzi yake kusudi ajitoe hivi leo kwa Yawe?” Basi wakubwa wa ukoo, viongozi wa makabila ya Israeli, majemadari wa maelfu na wa mamia; vilevile na wakubwa wasimamizi wa kazi za mufalme walipotoa kwa mapenzi yao, walitoa kwa ajili ya kazi za nyumba ya Mungu: toni mia moja makumi saba za zahabu, vikoroti elfu kumi vya zahabu, na zaidi ya toni mia tatu za feza, yapata toni mia sita za shaba, na zaidi ya toni elfu mia tatu za chuma. Wale ambao walikuwa na mawe ya bei kali wakayatoa kusudi yawekwe katika hazina ya nyumba ya Yawe, chini ya uangalizi wa Yehieli, Mugersoni. Halafu watu wakafurahi kwa sababu walitoa kwa mapenzi yao, maana kwa moyo wao wote walimutolea Yawe kwa mapenzi yao, naye mufalme Daudi akafurahi sana. Halafu Daudi akamutukuza Yawe mbele ya mukutano wote, akisema: “Utukuzwe milele na milele, ee Yawe, Mungu wa baba yetu Israeli. Ukubwa ni wako, ee Yawe, una nguvu, utukufu, ushindi na mamlaka. Vyote vinavyokuwa mbinguni na katika dunia ni vyako. Ee Yawe, ufalme ni wako, nawe umetukuzwa, uko mukubwa juu ya vitu vyote. Utajiri na heshima vinatoka kwako, vyote unavitawala. Uwezo na nguvu viko katika mukono wako, nawe unawatukuza wale unaowapenda, na kuwaimarisha wote. Sasa, ee Mungu wetu, tunakushukuru na kusifu jina lako tukufu. “Lakini, mimi ni nani, na watu wangu ni nani, hata tuweze kutoa kwa mapenzi yetu hivi? Kwa maana vitu vyote vinatoka kwako, tumekutolea vitu vinavyokuwa vyako wewe mwenyewe. Sisi tuko wageni mbele yako, na wasafiri kama vile babu zetu walivyokuwa wote. Siku zetu katika dunia ni kama kivuli kinachopita, hapa hakuna tumaini la kukaa. Ee Yawe, Mungu wetu, wingi wote huu tuliotoa kwa kukujenga nyumba kwa ajili ya utukufu wa jina lako takatifu, unatoka katika mukono wako na yote ni yako. Ninajua, Mungu wangu, kwamba wewe unapima moyo, nawe unapendezwa na uaminifu. Nami, katika uaminifu wa moyo wangu nimetoa vitu hivi vyote kwa mapenzi yangu, na sasa ninaona watu wako wanaokuwa hapa, wakikutolea kwa mapenzi yao na furaha. Ee Yawe, Mungu wa Abrahamu, Isaka na Israeli, babu zetu, ulinde mupango wa namna hiyo na mafikiri ya namna hiyo ndani ya mioyo ya watu wako, na uelekeze mioyo ya watu wako kwako. Umujalie Solomono mwana wangu kusudi kwa moyo wote ashike amri zako, ushuhuda na maagizo yako, atimize yote na apate kujenga nyumba hii ya utukufu niliyoifanyia matayarisho.” Kisha, mufalme Daudi akawaambia wote waliokusanyika: “Mumusifu Yawe, Mungu wenu.” Na wote waliokusanyika wakamutukuza Yawe, Mungu wa babu zao, wakainama mbele yake na kumwabudu Yawe na kumutolea mufalme Daudi heshima. Wakamutolea Yawe sadaka. Kesho yake wakamutolea sadaka za kuteketezwa kwa moto: ngombe dume elfu moja, wana-kondoo elfu moja, pamoja na sadaka zao za vinywaji na sadaka nyingi kwa ajili ya Waisraeli wote. Basi siku ile wakakula na kunywa kwa furaha kubwa mbele ya Yawe. Kwa mara ya pili wakamuweka Solomono mwana wa Daudi kuwa mufalme. Wakamupakaa mafuta apate kuwa mutawala katika jina la Yawe, na Zadoki akuwe kuhani. Halafu Solomono akaikaa katika kiti cha kifalme cha Yawe, kwa pahali pa baba yake Daudi. Naye akafanikiwa; na taifa lote la Waisraeli likamutii. 29.23 Ang. 1 Fal 2.12 Viongozi wote na mashujaa vilevile na wana wote wa mufalme Daudi, wakaahidi kuwa watiifu kwa mufalme Solomono. Yawe akamupa Solomono sifa nzuri mbele ya Waisraeli wote, akamupa utukufu wa kifalme unaopita utukufu wa mufalme yeyote aliyeitawala inchi ya Israeli mbele yake. Basi Daudi, mwana wa Yese, akakuwa mufalme juu ya inchi yote ya Israeli. Na muda aliotawala juu ya inchi ya Israeli ulikuwa miaka makumi ine; miaka saba alitawala akiwa Hebroni na miaka makumi tatu na mitatu alitawala akiwa Yerusalema. Alikufa akiwa muzee sana, alishiba siku, akiwa na mali na heshima. Mwana wake Solomono akakuwa mufalme kwa pahali pake. Solomono, mwana wa mufalme Daudi, alijiimarisha katika utawala wake, naye Yawe, Mungu wake akamubariki na kumufanya akuwe mukubwa sana. Mufalme Solomono aliita majemadari wote wa vikundi vya maelfu na vya mamia, waamuzi, viongozi wote wa ukoo za Waisraeli. Kisha akaandamana nao mpaka pahali pa ibada kule Gibeoni. Walikwenda kule kwa sababu pale ndipo pahali palipokuwa hema la mukutano la Mungu ambalo Musa mutumishi wa Yawe, alilotengeneza katika jangwa. (Lakini, sanduku la Mungu lilikuwa Yerusalema katika hema ambalo mufalme Daudi alilipigia alipolileta kutoka Kiriati-Yearimu). Tena, mazabahu ya shaba iliyotengenezwa na Bezaleli, mwana wa Uri na mujukuu wa Huri, ilikuwa kule Gibeoni mbele ya hema takatifu la Yawe. Hapo mufalme Solomono na watu wote wakamwomba Yawe. Solomono akapanda mbele ya mazabahu ya shaba iliyokuwa kwenye hema la mukutano. Pale mbele ya Yawe, akatoa sadaka elfu moja za kuteketezwa juu ya mazabahu yale. Usiku ule, Mungu akamutokea Solomono, akamwambia: “Omba kitu chochote unachotaka, nami nitakupa.” Solomono akamwambia Mungu: “Ulimutendea baba yangu Daudi mema mengi, na umenijalia kuwa mufalme kwa pahali pake. Sasa, ee Mungu, Yawe, utimize ahadi uliyomupa Daudi baba yangu. Umeniweka kuwa mufalme juu ya watu hawa wanaokuwa wengi kama mavumbi. Kwa hiyo, ninakuomba unipe hekima na maarifa kusudi niweze kuwatawala watu wako vizuri. Kama sivyo, nitaweza namna gani kuwatawala hawa watu wako wanaokuwa wengi hivi?” Mungu akamujibu Solomono: “Kwa sababu jambo hili uliloomba liko ndani ya moyo wako, na wala haukuomba mali, wala utajiri, wala heshima wala haukuomba wanaokuchukia waangamizwe, wala maisha marefu, lakini umeomba hekima na maarifa kusudi uwatawale vizuri watu wangu ambao nimekupa ukuwe mufalme wao, ninakupa hekima na maarifa. Vilevile, nitakupa utajiri, mali na heshima zaidi ya mufalme mwingine yeyote aliyekuwa mbele yako na mufalme mwingine yeyote atakayetawala nyuma yako.” Basi, Solomono akaondoka pahali pale pa kuabudia, kule Gibeoni, kulipokuwa hema la mukutano, akarudi Yerusalema. Akatawala inchi ya Israeli. Solomono alikusanya magari ya vita na waaskari wapanda-farasi; alikuwa na magari ya vita elfu moja na mia ine, na waaskari wapanda-farasi elfu kumi na mbili. Aliwaweka katika miji yenye vituo vya magari ya vita na kwake katika Yerusalema. Mufalme Solomono aliongeza feza na zahabu zikakuwa nyingi kama mawe katika Yerusalema, na mbao za mierezi zikapatikana kwa wingi kama mikuyu ya Sefela. Farasi wa Solomono walitoka Misri na Kilikia; wachuuzi wake waliwanunua toka kule. Walinunua gari moja la vita kutoka Misri kwa bei ya vikoroti mia sita za feza, na farasi mumoja kwa vikoroti mia moja na makumi tano za feza. Kisha waliwauzishia wafalme wa Wahiti na wa Wasuria farasi hao na magari. Mufalme Solomono akakusudia kujenga nyumba ambamo Yawe ataabudiwa, na vilevile kujijengea yeye mwenyewe nyumba ya kifalme. Akapanga wanaume elfu makumi saba kuwa wabebaji wa mizigo, elfu makumi nane kuwa wachongaji wa mawe kwenye milima na wengine elfu tatu mia sita kuwa wasimamizi wao. Kisha, Solomono akatuma ujumbe kwa Hiramu, mufalme wa Tiro, akamwambia: “Unitendee na mimi kama vile ulivyomutendea baba yangu Daudi, ulipomupelekea mierezi ya kujenga nyumba ya kifalme. Ninataka kujenga nyumba ya kumwabudia Yawe wangu. Nitaitakasa kwa ajili yake, nayo itakuwa pahali pa kufukiza ubani wenye harufu nzuri mbele yake, na vilevile pahali pa kumutolea mikate mitakatifu siku zote, na sadaka za kuteketezwa asubui na magaribi na za siku za Sabato, za Mwandamo wa Mwezi, na sikukuu zingine za Yawe, Mungu wetu, kama vile alivyoagiza Waisraeli milele. Nyumba ninayokusudia kujenga itakuwa kubwa sana, maana Mungu wetu ni mukubwa zaidi ya miungu yote. Lakini ni nani anayeweza kumujengea nyumba ikiwa mbingu zenyewe hazimutoshi, wala mbingu za juu sana? Nami ni nani basi, hata nimujengee nyumba isipokuwa tu kama pahali pa kufukizia ubani mbele yake? Basi, sasa unitumie mutu mwenye ujuzi wa kutengeneza vyombo kwa zahabu, feza, shaba, na chuma, na nguo ya rangi nyekundu-nyeusi, za rangi nyekundu na ya samawi, anayejua vilevile kuchora. Yeye atashirikiana katika kazi hiyo na wafundi wanaokuwa pamoja nami katika Yuda na Yerusalema, ambao baba yangu Daudi aliwaweka. Tena unitumie miti ya mierezi, miberoshi na musandali kutoka Lebanoni, kwa maana ninajua kwamba watumishi wako ni hodari sana wa kupasua mbao kule Lebanoni. Nao watumishi wangu watashirikiana na watumishi wako, kusudi wanipasulie mbao kwa wingi, maana nyumba ninayokusudia kujenga ni kubwa na ya ajabu. Kwa ajili ya watumishi wako, ni kusema waseremala watakaopasua mbao, nitatoa toni mia mbili za ngano iliyopondwa, toni mia mbili za shayiri, litre elfu mia ine za divai na litre elfu mia ine za mafuta.” Naye Hiramu, mufalme wa Tiro, akamujibu Solomono kwa barua akisema: “Kwa sababu Yawe anawapenda watu wake, amekufanya kuwa mufalme wao. Atukuzwe Yawe, Mungu wa Israeli, aliyeumba mbingu na dunia! Amemupa mufalme Daudi mwana mwenye hekima, ufahamu na akili, atakayemujengea Yawe nyumba, na kujijengea nyumba ya kifalme. Sasa ninakutumia fundi mwenye ujuzi sana na mwenye akili, jina lake Huruma-Abi. Mama yake ni wa kabila la Dani, na baba yake ni wa Tiro. Yeye ana ujuzi mwingi wa kazi ya zahabu, feza, shaba, chuma, mawe, miti, nguo ya rangi nyekundu-nyeusi, ya samawi, ya nyekundu na ya kitani safi. Tena ni hodari na anaweza kuchora kila aina ya michoro kufuatana na maelezo yoyote ambayo angepewa. Yeye atafanya kazi pamoja na wafundi wako, wafundi wa bwana wangu, Daudi baba yako. Sasa basi, bwana wangu, tafazali ututumie sisi watumishi wako vitu ulivyosema: ngano, shayiri, mafuta na divai. Nasi tutapasua mbao kadiri ya mahitaji yako kutoka kule Lebanoni. Kisha tutazifunga pamoja kwa njia ya bahari zielee mpaka Yopa. Kutoka kule utazipeleka Yerusalema.” Mufalme Solomono akawahesabu wageni wote waliokuwa katika inchi ya Israeli. Hesabu hii ni kama ile Daudi baba yake aliyofanya. Kulikuwa wageni yapata elfu mia moja makumi tano na tatu na mia sita. Kati yao akawapa watu elfu makumi saba kazi ya kubeba mizigo, watu elfu moja wakakuwa wachongaji wa mawe kwenye milima, na watu elfu tatu mia sita wakakuwa wasimamizi kusudi wawasukume watu kufanya kazi. Kisha Solomono akaanza kujenga nyumba ya Yawe katika Yerusalema juu ya mulima Moria ambapo Yawe alimutokea Daudi baba yake, pahali ambapo Daudi alikuwa amepachagua, kwenye kiwanja cha kupepetea ngano cha Ornani Muyebusi. Mufalme Solomono akaanza kujenga hekalu katika mwezi wa pili wa mwaka wa ine wa utawala wake. Vipimo Solomono alivyotumia kwa kujenga nyumba ya Mungu, vilikuwa kama hivi: urefu metre makumi mbili na saba na upana metre kenda. Chumba cha sehemu ya kuingilia kilikuwa na urefu wa metre kenda, sawa na upana wa nyumba hiyo, na urefu kwenda juu metre makumi tano na ine. Kuta zake zilifunikwa kwa zahabu safi upande wa ndani. Baraza ilifunikwa kwa mbao za miberoshi. Kisha kwa zahabu safi na kuchorwa mifano ya miti ya ngazi na minyororo. Mufalme Solomono aliipamba nyumba ya Yawe kwa mawe mazuri ya bei kali. Zahabu aliyotumia ilitoka katika inchi ya Parawaimu. Alipakaa nyumba yote zahabu; nguzo zake, vizingiti vyake, kuta zake na milango yake. Vilevile wakachora kwenye kuta sanamu za makerubi. Tena, alipatengeneza Pahali Patakatifu Sana. Urefu wake ulikuwa metre kenda, sawasawa na upana wake ambao vilevile ulikuwa metre tisa. Alitumia zaidi ya toni makumi mbili za zahabu kwa kupakaa ndani ya chumba kile. Misumari aliyoitumia ilikuwa ya uzito wa grama mia tano na makumi saba za zahabu. Vilevile alipakaa vyumba vyote vya gorofi kwa zahabu. Akatengeneza sanamu mbili za makerubi kwa mbao, akazipakaa kwa zahabu na kuziweka katika Pahali Patakatifu Sana. Kila kerubi ilikuwa na mabawa mawili yenye urefu wa metre ine na nusu kwa jumla, metre mbili na sentimetre makumi mbili na tano kila bawa. Bawa moja liligusa ukuta upande mumoja wa chumba na la pili liligusana na la kerubi wa pili. Vilevile bawa moja la kerubi wa pili liligusa ukuta upande mwingine wa chumba na la pili likagusana na la kerubi wa kwanza katikati ya chumba. Urefu wa mabawa mawili ya makerubi hawa ni metre ine na nusu. Yalisimama yakielekana, nyuso za makerubi zikielekea kwenye baraza. Akatengeneza pazia kwa kitambaa cha kitani safi, cha rangi ya samawi, ya rangi nyekundu-nyeusi na nyekundu. Akalichora kwa michoro ya makerubi. Mufalme Solomono alitengeneza nguzo mbili za shaba, kila moja yenye urefu wa metre mia moja kumi na tano na nusu, akaziweka mbele ya nyumba. Kisha akatengeneza taji mbili, kila moja yenye urefu wa metre mbili na sentimetre makumi mbili na tano, akaziweka juu ya nguzo zile. Alitengeneza minyororo kwa mufano wa mikufu, akaiweka juu ya vichwa vya nguzo hizo, kisha akatengeneza mifano ya matunda aina ya makomamanga mia moja, akayaweka juu ya minyororo hiyo. Akazisimamisha nguzo zile kwenye baraza ya hekalu, moja upande wa kusini, na ingine upande wa kaskazini; ile ya upande wa kusini akaiita Yakini, na ya upande wa kaskazini akaiita Boazi. Mufalme Solomono alitengeneza birika la maji la muviringo lenye urefu wa metre mbili na sentimetre makumi mbili na tano na upana sawa na metre kenda, na urefu wake kwenda juu metre ine na nusu. Kisha, akatengeneza birika la maji la muviringo, lenye upana wa metre ine na nusu kutoka ukingo mpaka ukingo, lenye urefu wa metre mbili na sentimetre makumi mbili na tano, na lenye muzunguko wa metre kumi na tatu na nusu. Chini ya ukingo wake, kuzunguka lile birika, kulikuwa mistari miwili ya sanamu za ngombe dume, kwa metre kumi na tatu na nusu. Sanamu hizo za ngombe dume zilikuwa zimetengenezwa na shaba ileile wakati birika lilipofanywa. Nalo birika lilikuwa limewekwa juu ya sanamu za ngombe dume kumi na wawili, tatu zikielekea upande wa kaskazini, tatu upande wa magaribi, tatu kusini na zingine tatu upande wa mashariki. Unene wa ukingo wake ulikuwa sentimetre saba na nusu. Ukingo wake ulikuwa kama ukingo wa kikombe, na kama maua ya yungiyungi. Ndani ya birika lile kuliweza kuingia kadiri ya litre elfu makumi sita za maji. Akatengeneza vilevile beseni kumi za kusafishia sehemu za nyama zilizotumika katika sadaka za kuteketezwa kwa moto. Tano kati ya bakuli zile akaziweka upande wa kusini na tano upande wa kaskazini. Birika lilitumiwa na makuhani kwa kunawia. Alitengeneza vinara kumi vya zahabu kama vile ilivyoagizwa, akaviweka katika baraza ya hekalu; vitano upande wa kusini, na vitano upande wa kaskazini. Akatengeneza vilevile meza kumi, nazo akaziweka ndani ya chumba cha hekalu. Kisha akatengeneza beseni mia moja za zahabu. Akatengeneza kiwanja cha ndani cha makuhani na kingine kikubwa cha inje, na milango ya kiwanja ambayo aliifunika na shaba; na lile birika akaliweka kwenye pembe ya kusini-mashariki ya nyumba. Hiramu akatengeneza vyungu, vipao na mabeseni. Basi Hiramu akamaliza kazi aliyomufanyia mufalme Solomono juu ya nyumba ya Mungu; nguzo mbili, mabakuli, taji mbili juu ya nguzo, na nyavu mbili kwa ajili ya kufunika mabakuli ya taji zilizowekwa juu ya nguzo; vilevile mifano ya makomamanga mia ine kwa ajili ya nyavu zile mbili, mistari miwili miwili ya makomamanga kwa kila wavu, kwa kupamba mabakuli yale mawili ya taji zilizokuwa juu ya kila nguzo. Vilevile akatengeneza beseni juu ya magari, na birika lile moja, na sanamu za ngombe dume kumi na wawili chini ya birika lile. Halafu vyungu, vipao na kanya na vyombo vingine vyote vya nyumba ya Yawe ambavyo Huruma-Abi alimutengenezea mufalme Solomono, vilikuwa vya shaba iliyoangarishwa. Vitu hivyo vyote mufalme alivitengeneza katika kiwanja cha Yordani, sehemu ya udongo wa mufinyanzi iliyokuwa kati ya Sukoti na Sereda. Uzito wa shaba iliyotumiwa kwa kutengeneza vyombo hivi haukujulikana kwa maana Solomono alitengeneza vyombo vingi sana. Solomono alitengeneza vitu vyote vilivyokuwa katika nyumba ya Mungu: mazabahu ya zahabu na meza za mikate mitakatifu; vinara na taa za zahabu safi za kuangazia Pahali pale Patakatifu Sana, kama vile walivyoamuriwa; maua, taa na koleo, vyote vikiwa vya zahabu safi kabisa; makasi na mabeseni, sahani za kuwekea ubani na vyetezo vya kubebea moto, vyote vya zahabu safi, pete za hekalu za milango ya Pahali Patakatifu Sana, na za milango mingine ya vyumba vya ndani, zote zilitengenezwa na zahabu. Basi, Solomono akamaliza kazi zote zilizoelekea nyumba ya Yawe. Kisha Solomono akaleta mali yote baba yake Daudi aliyokuwa ameitoa kwa Mungu, ni kusema: feza, zahabu na vyombo; akaiweka katika hazina za nyumba ya Mungu. Basi mufalme Solomono akawakusanya kule Yerusalema wazee na viongozi wote wa makabila wa ukoo za Waisraeli kusudi waondoe Sanduku la Agano la Yawe kutoka katika muji wa Daudi, ni kusema Sayuni. Halafu wote wakakutana mbele ya mufalme katika sikukuu ya mwezi wa saba. Nyuma ya wazee wote wa Waisraeli kufika, Walawi wakabeba Sanduku la Agano, Walawi na makuhani wakahamisha Sanduku la Agano na hema la mukutano na vyombo vitakatifu vyote vilivyokuwa mule ndani ya hema. Mufalme Solomono na mukutano wa Waisraeli wakakusanyika mbele ya Sanduku la Agano nao wakatoa sadaka ya ngombe na kondoo wasiohesabika. Kisha makuhani wakaingiza Sanduku la Agano la Yawe pahali pake, katika chumba cha ndani cha nyumba, Pahali Patakatifu Sana, chini ya mabawa ya makerubi. Wale makerubi walitandaza mabawa yao juu ya pahali palipowekwa sanduku, kwa hiyo sanduku na miti yake ya kulibebea vilikuwa chini ya mabawa. Kwa sababu miti ile ilikuwa mirefu sana, incha zake ziliweza kuonekana kutoka Pahali Patakatifu mbele ya chumba cha ndani, lakini haikuweza kuonekana kutoka upande wa inje. Miti ile ingali pahali pale hata leo. Ndani ya Sanduku la Agano, hamukukuwa kitu kingine isipokuwa tu vile vibao viwili ambavyo Musa aliviweka mule kule Horebu, pahali Yawe alipofanya agano na watu wa Israeli, walipotoka Misri. Kisha makuhani wakatoka pale Pahali Patakatifu, kwa sababu makuhani wote waliokuwa pale bila kujali makundi yao, walikuwa wamejitakasa. Walawi wote waimbaji, pamoja na Asafu, Hemani, na Yedutuni, pamoja na Walawi wengine wa ukoo zao, wakiwa wamevaa nguo zao za kitani safi nao wakabeba matoazi, vinanda na vinubi, walisimama upande wa mashariki wa mazabahu. Makuhani mia moja na makumi mbili wapiga baragumu walikuwa pamoja nao. Waimbaji na wapiga baragumu wote pamoja walitoa sauti kwa pamoja na matoazi na vyombo vingine vya muziki, wakimusifu Yawe wakiimba: “Yeye ni muzuri. Wema wake unadumu milele.” Wakati ule nyumba ya Yawe ikajazwa na wingu. Nao makuhani walishindwa kutumika kwa sababu ya wingu lile, maana utukufu wa Yawe ulijaza nyumba ya Mungu. Halafu Solomono akasema: “Yawe alisema kwamba atakaa katika giza kubwa. Hakika nimekujengea nyumba tukufu kuwa makao yako ya milele.” Kisha Solomono akageukia mukutano wote wa watu wa Israeli wakiwa wanasimama akawabariki. Akasema: “Atukuzwe Yawe, Mungu wa Israeli, maana kwa nguvu zake ametimiza ahadi yake aliyoitoa kwa baba yangu Daudi akisema: ‘Tangu nilipowaondoa watu wangu kutoka inchi ya Misri, sikuchagua muji wowote katika makabila ya Waisraeli kusudi nijengewe nyumba nitakamoabudiwa; na sikumuchagua mutu yeyote akuwe mukubwa wa watu wangu Waisraeli. Lakini kisha nilichagua muji wa Yerusalema ukuwe muji ambamo nitaabudiwa, na nilimuchagua Daudi awatawale watu wangu Waisraeli.’ “Kwa hiyo, baba yangu Daudi alikusudia kujenga nyumba ambamo Yawe, Mungu wa Israeli, atakamoabudiwa. Lakini Yawe alimwambia baba yangu Daudi: ‘Ni vizuri kwamba ulikusudia ndani ya moyo wako kunijengea nyumba. Hata hivyo, si wewe utakayejenga nyumba, lakini mwana wako utakayemuzaa ndiye atakayenijengea ile nyumba.’ ” “Na sasa Yawe ametimiza ahadi yake, maana nimekuwa mufalme kwa pahali pa baba yangu Daudi, na kuikaa juu ya kiti cha kifalme cha Israeli kama vile Yawe alivyoahidi; tena nimejenga nyumba ya kumwabudia Yawe, Mungu wa Israeli. Katika nyumba hiyo nimeweka Sanduku la Agano, ambalo ndani yake kuna agano la Yawe alilofanya na watu wa Israeli.” Kisha, Solomono akasimama mbele ya mazabahu ya Yawe, halafu mbele ya mukutano wote wa watu wa Israeli, akainua mikono yake juu. Solomono alikuwa ametengeneza mimbari ya shaba ambayo aliweka katikati ya kiwanja. Urefu na upana wake ulikuwa metre mbili na sentimetre makumi mbili na tano, na urefu kwenda juu metre moja na sentimetre makumi mbili na tano. Akapanda juu ya mimbari na kupiga magoti mbele ya watu wote wa Israeli, akainua mikono yake kuelekea mbinguni. Aliomba akisema: “Ee, Yawe, Mungu wa Israeli, hakuna Mungu mwingine kama wewe, mbinguni au katika dunia. Wewe ni mwaminifu, maana umetimiza agano lako na kutenda mema kwa watumishi wako wanaoishi wakikutii kwa moyo wao wote. Umetimiza ahadi uliyotoa kwa mutumishi wako baba yangu Daudi, kweli, yale uliyosema umeyatimiza leo kwa uwezo wako mwenyewe. “Kwa hiyo sasa, Ee Yawe, Mungu wa Israeli, ninakuomba tena utimize ile ahadi uliyomwahidi mutumishi wako Daudi baba yangu, ukisema: ‘Siku zote utakuwa na mutu wa uzao wako wa kuikaa katika kiti cha kifalme cha Israeli, ikiwa wazao wako wataangalia mwenendo na kushika sheria zangu kama vile wewe ulivyofanya mbele yangu.’ Sasa, ee Yawe, Mungu wa Israeli, ninakusihi utimize yote uliyomwahidi mutumishi wako Daudi. “Lakini, ee Mungu kweli utakaa humu katika dunia na wanadamu, ikiwa hata mbingu zenyewe, wala mbingu za mbingu za juu sana hazikutoshi? Namna gani nyumba hii ambayo nimejenga itakutoshelea? Hata hivyo, ee Yawe, Mungu wangu, mimi mutumishi wako, ninakuomba unisikilize na kunitimizia ombi langu ninaloomba leo. Uchunge nyumba hii muchana na usiku pahali ambapo umechagua watu wako waliabudie jina lako. Unisikilize mimi mutumishi wako ninapokuja pahali hapa kuomba. Sikia maombi yangu mimi mutumishi wako na ya watu wako Waisraeli wanapoomba wakielekea pahali hapa. Usikilize maombi kutokea kule mbinguni na ukisha kusikia, usamehe. “Mutu akimukosea mwenzake, naye akiletwa apate kuapa mbele ya mazabahu yako katika nyumba hii, na akiapa tafazali wewe usikilize kutokea kule mbinguni, utende na kuwahukumu watumishi wako. Anayekuwa na kosa umwazibu kadiri ya makosa yake; asiyekuwa na kosa umwachilie na kumupatia haki kadiri ya uhaki wake. “Wakati watu wako Waisraeli watakaposhindwa na waadui zao, kwa sababu ya zambi walizotenda mbele yako, nao wakitubu kwako na kusifu jina lako, wakiomba musamaha wako kwa unyenyekevu, katika nyumba hii, basi, usikilize kutokea kule mbinguni. Usamehe zambi zao na uwarudishe katika inchi uliyowapa wao na babu zao. “Mvua isiponyesha kwa sababu wametenda zambi mbele yako, wakiomba wakielekea pahali hapa na kusifu jina lako, tena wakiacha zambi zao, tafazali uwasikilize kutokea kule mbinguni, na usamehe zambi za watumishi wako watu wako Waisraeli, nawe ukiwafundisha kufuata njia nzuri, unyeshe mvua katika inchi yako hii ambayo uliwapa watu wako ikuwe urizi. “Ikiwa kuna njaa katika inchi au ugonjwa mukali, ukosefu wa mvua, ugonjwa wa mimea, nzige au vidudu vingine, au ikiwa watu wako wakishambuliwa na waadui zao katika muji wao wowote, ikiwa kuna pigo lolote au ugonjwa wowote, tafazali usikilize maombi yoyote yatakayoombwa na mutu yeyote au watu wako wote Waisraeli, kila mutu akijua taabu yake na huzuni yake akikuomba naye akinyoosha mikono yake kuelekea nyumba hii, basi usikilize kutokea kule mbinguni, utoe musamaha, vilevile umutendee kila mutu kadiri anavyostahili, (maana ni wewe tu unayejua mawazo ya mioyo ya wanadamu wote), kusudi wakutii na kwenda katika njia zako wakati wote wanapoishi katika inchi uliyowapa babu zetu. “Na hata mugeni asiyekuwa Mwisraeli atakayekuja kutoka inchi ya mbali kwa ajili ya jina lako kubwa, na juu ya nguvu na ulinzi wako, akikuja kuomba katika nyumba hii, ninakusihi umusikilize toka kule kwako mbinguni, na umujalie yule mugeni yote atakayokuomba kusudi watu wote katika ulimwengu wapate kujua jina lako na kukutii kama vile watu wako Waisraeli walivyofanya na wapate kufahamu kwamba nyumba hii ambayo nimejenga inajulikana kwa jina lako. “Watu wako wakienda kwenye vita kupigana na waadui zao kokote kule utakakowapeleka, nao wakikuomba wakielekea muji huu uliochagua na nyumba ambayo nimejenga kwa ajili ya jina lako, ninakusihi usikilize maombi yao na malalamiko yao ukiwa kule mbinguni na uwapatie ushindi katika vita. “Ikiwa watatenda zambi mbele yako, maana hakuna mutu asiyetenda zambi, na ukiwakasirikia na kuwaacha washindwe na waadui, hata wapelekwe kuwa watumwa mpaka inchi ya mbali au ya karibu, kama watakapokuwa kule katika uhamisho watajifikiri kwa roho yao yote na kwa moyo wao wote na kutubu na kukuomba musamaha, wakisema: ‘Tumetenda zambi; tumepotoka na kufanya maovu’, tena kama watatubu kwa moyo wao wote na kwa roho yao yote wakati watakapokuwa katika inchi ya uhamisho, na kama watakuomba wakielekea inchi yao ambayo uliwapatia babu zao, muji huu ambao uliuchagua na nyumba hii ambayo nimeijenga kwa ajili ya jina lako, basi, ninakusihi usikilize ukiwa kule mbinguni maombi yao na malalamiko yao na uwapatie haki zao tena uwasamehe watu wako ambao wametenda zambi mbele yako. “Sasa ee Mungu wangu, utuangalie na upokee maombi tutakayoomba pahali hapa. “Sasa, ee Yawe, Mungu, uingie pahali pako pa kupumzika, wewe pamoja na Sanduku la Agano la nguvu zako. “Ee Yawe, Mungu, makuhani wako wapate wokovu, na watakatifu wako wafurahie uzuri wako. “Ee Yawe, Mungu, usimugeuzie masiya wako mugongo. Kumbuka wema wako kwa mutumishi wako Daudi.” Solomono alipomaliza maombi yake, moto ukashuka kutoka mbinguni na kuchoma sadaka na sadaka za kuteketeza kwa moto zilizotolewa, kisha utukufu wa Yawe ukajaza nyumba. Makuhani hawakuweza kuingia mule kwa sababu utukufu wa Yawe ulijaa nyumba ya Yawe. Waisraeli wote walipoona moto ukishuka kutoka mbinguni na utukufu wa Yawe katika nyumba, wakainama nyuso zao zikifika mpaka chini. Wakamwabudu na kumushukuru Yawe wakisema: “Yeye ni muzuri. Wema wake unadumu milele.” Kisha mufalme Solomono na watu wote wakamutolea Yawe sadaka. Naye Solomono akamutolea ngombe elfu makumi mbili na mbili na kondoo elfu mia moja makumi mbili. Hivi ndivyo Solomono na watu wote walivyozinduwa nyumba ya Mungu. Makuhani walikuwa wakisimama kwenye nafasi za kazi zao, nao Walawi, walisimama wakiwa na vyombo vya Yawe vya muziki mufalme Daudi alivyotengeneza kwa ajili ya kutoa shukrani kwa Yawe. Waliimba: “Wema wake unadumu milele.” Wakati Daudi alipotoa shukrani, walimusaidia; makuhani walipiga baragumu nao Waisraeli wote wakasimama. Basi, mufalme Solomono akazindua sehemu ya katikati ya kiwanja kilichokuwa mbele ya nyumba ya Yawe, maana ni pale ndipo alipotolea sadaka za kuteketezwa kwa moto na mafuta ya sadaka za amani, kwa sababu ile mazabahu ya shaba haikutosha kwa sadaka zile zote. Naye Solomono kwa muda wa siku saba alifanya sikukuu pamoja na kusanyiko kubwa la watu wote wa Israeli waliotoka kwenye kiingilio cha Hamati mpaka kwenye muto wa Misri. Siku ya nane, walikusanyika wakafanya sikukuu nyuma ya muda wa siku saba, walizotumia kwa kutakasa meza ya matoleo ya sadaka, na siku saba nyingine za sikukuu. Siku iliyofuata ambayo ilikuwa siku ya makumi mbili na tatu ya mwezi wa saba, Solomono akawaaga watu waende kwao, wakishangilia na kufurahi ndani ya moyo kwa sababu ya mazuri ambayo Yawe alimutendea Daudi, Solomono na kwa watu wake Waisraeli. Basi, mufalme Solomono akamaliza kujenga nyumba ya Yawe na nyumba ya kifalme na kutimiza yale yote aliyokusudia kuifanyia nyumba ya Yawe na nyumba ya kifalme. Kisha Yawe akamutokea usiku, akamwambia: “Nimesikia maombi yako na nimechagua pahali hapa pakuwe nyumba yangu ya kunitolea sadaka. Nikiwanyima mvua au nikiwaletea nzige wakule mimea yao au nikiwapiga kwa ugonjwa mukali kama watu wangu hao wakijinyenyekeza, wakiomba, wakinitafuta na kuacha njia zao mbaya, basi, mimi nitawasikiliza kutokea juu mbinguni, nitawasamehe zambi yao na kustawisha inchi yao. Sasa nitachunga hekalu hili na kusikiliza maombi yatakayofanyika hapa, kwa maana nimetakasa nyumba hii kusudi watu waliabudu jina langu hapa milele. Nitailinda na kuipenda siku zote. Nawe kama ukinitumikia kwa uaminifu kama vile Daudi baba yako alivyofanya, ukitenda yote niliyokuamuru na kutii maongozi yangu na maagizo yangu, basi, mimi nitaimarisha kiti chako cha kifalme kama nilivyofanya agano na Daudi baba yako nikisema: ‘Hautakosa mutu wa kutawala inchi ya Israeli.’ “Lakini mukiacha kunifuata, na kuasi maongozi yangu na amri nilizowapa, na kwenda kutumikia miungu mingine na kuiabudu, kwa sababu hiyo mimi nitawaongoa kutoka katika inchi hii ambayo nimewapa. Vielvile na nyumba hii ambayo nimeitakasa kwa ajili ya jina langu nitaitupilia mbali nami, na kuifanya kitu cha kuchekelewa na kuzarauliwa kati ya mataifa yote.” “Na juu ya nyumba hii ambayo nimetukuzwa, kila anayepita karibu atashituka na kuuliza: ‘Kwa nini Yawe amefanya hivyo kwa inchi hii na kwa nyumba hii?’ Watu wengine watajibu: ‘Ni kwa sababu walimwacha Yawe, Mungu wa babu zao aliyewatoa toka katika inchi ya Misri; wakashikamana na miungu mingine, wakaiabudu na kuitumikia. Kwa hiyo Yawe amewaletea hasara hizi zote.’ ” Kisha miaka makumi mbili, ambayo Solomono alipitisha kwa kujenga nyumba ya Yawe na nyumba ya kifalme, Solomono akajenga upya miji aliyopewa na Hiramu, halafu akawapa Waisraeli miji hiyo waishi mule. Nyuma ya pale Solomono akaenda katika muji wa Hamati-Soba na kuuteka, na kuujenga muji wa Tadimori katika jangwa. Alijenga upya miji ya gala iliyokuwa kule Hamati. Vilevile, Solomono akajenga miji hii: Beti-Horoni wa juu, na Beti-Horoni wa chini, miji yenye minara ya kufichamia, kuta, milango na vifungio, muji wa Balati, na miji yake yote ya kuwekea magari yake ya vita na ya waaskari wapanda-farasi wake, na kitu chochote alichotaka kujenga katika Yerusalema, Lebanoni au nafasi ingine katika ufalme wake. Watu wengine wote waliobaki kati ya Wahiti, Waamori, Waperizi, Wahivi na Wayebusi, ni kusema wote ambao hawakukuwa Waisraeli, vilevile kati ya wazao wao ambao Waisraeli hawakuwaangamiza, Solomono akawatumikisha kazi za kulazimishwa, na hivi ndivyo wanavyofanya hata sasa. Lakini kati ya watu wa Israeli, Solomono hakumufanya mutu yeyote kuwa mutumwa; kwa ajili ya kazi yake: wao walikuwa waaskari, majemadari wa wakubwa wake, majemadari wa magari yake ya vita na waaskari wapanda-farasi wake. Hii ndiyo jumla ya wakubwa wa mufalme Solomono: walikuwa mia mbili makumi tano, waliokuwa na mamlaka juu ya watu. Solomono alimuhamisha binti wa mufalme wa Misri, kutoka muji wa Daudi, akamupeleka kwenye nyumba aliyomujengea. Akasema: “Muke wangu hataishi katika nyumba ya Daudi mufalme wa Israeli, kwa maana pahali pote ambapo sanduku la Yawe limekuwa, ni patakatifu.” Solomono akamutolea Yawe sadaka za kuteketeza juu ya mazabahu aliyokuwa amemujengea Yawe mbele ya baraza la hekalu. Alitoa sadaka zile kadiri ilivyotakiwa na amri ya Musa kila siku takatifu, ni kusema siku za Sabato, sikukuu za mwandamo wa mwezi, na sikukuu tatu za kila mwaka – sikukuu ya Mikate Isiyotiwa Chachu, sikukuu ya majuma na sikukuu ya vibanda. Akifuata maagizo ya Daudi baba yake, alipanga zamu za kila siku za makuhani na za Walawi waliowasaidia makuhani kusifu na kutimiza kazi zao. Vilevile aliwapanga walinzi wa milango katika makundi aliyoweka kwa kulinda kila mulango; maana ndivyo Daudi, mutu wa Mungu alivyoamuru. Nao hawakuacha maagizo ya mufalme aliyowaamuru makuhani na Walawi kwa jambo lolote na juu ya hazina. Basi kazi zote Solomono alizokusudia kufanya zikamalizika. Yeye alitimiza kazi zile zote tangia jiwe la musingi wa nyumba ya Yawe lilipowekwa mpaka ilipomalizika kujengwa. Hivi nyumba ya Yawe ikamalizika. Kisha Solomono akakwenda Ezioni-Geberi na Eloti kwa vivuko vya bahari, katika inchi ya Edomu. Hiramu akamupelekea mashua zilizokuwa chini ya uongozi wa watumishi wake, pamoja na wafundi wa mashua. Wale, pamoja na watumishi wa Solomono, wakasafiri mpaka Ofiri, na kubeba kutoka kule zahabu, wakamuletea mufalme Solomono yapata kilo elfu kumi na tano. Malkia wa Seba aliposikia sifa za Solomono, basi akafika Yerusalema kwa kumujaribu Solomono kwa maulizo magumu. Alifika Yerusalema akisindikizwa na watu wengi sana, pamoja na ngamia waliobeba marasi, zahabu nyingi sana na mawe ya bei kali. Na alipofika kwa Solomono, akamwuliza maulizo yote aliyokuwa nayo ndani ya moyo wake. Solomono akajibu maulizo yote, hakukuwa jambo lolote aliloshindwa kumwelezea. Malkia wa Seba alishangaa sana kuona hekima ya Solomono, nyumba aliyokuwa ameijenga, chakula kilichotayarishwa kwenye meza yake, jinsi wakubwa wake walivyokaa kwenye meza, kazi ya watumishi wake na namna walivyovaa, wenye kuleta vinywaji na jinsi walivyovaa, na sadaka za kuteketeza ambazo alitoa katika nyumba ya Yawe. Akamwambia mufalme: “Yote niliyosikia katika inchi yangu juu ya kazi zako na hekima yako ni ya kweli! Lakini sikuweza kuamini habari zao mpaka nilipofika na kujionea mwenyewe, na kumbe niliambiwa nusu tu; hekima yako na fanaka ni zaidi ya yale niliyosikia. Heri kwa wake zako! Heri kwa hawa watumishi wako ambao wanasimama siku zote mbele yako na kusikiliza hekima yako! Na asifiwe Yawe, Mungu wako, ambaye amependezwa nawe, akakuikalisha juu ya kiti chake cha kifalme, ukuwe mufalme kwa jina la Yawe, Mungu wako. Kwa sababu Mungu wako amewapenda Waisraeli na kuwaimarisha milele, amekuweka wewe ukuwe mufalme juu yao kusudi uimarishe uhaki na sheria ya Mungu.” Kisha akamupa mufalme zaidi ya kilo elfu ine za zahabu, na kiasi kikubwa cha marasi na mawe ya bei kali. Aina ya marasi ambayo yule malkia wa Seba alimupatia mufalme Solomono, yalikuwa ya pekee. Vilevile, watumishi wa Hiramu pamoja na watumishi wa Solomono walioleta zahabu kutoka Ofiri, walileta vilevile miti ya musandali na mawe ya bei kali. Solomono alitumia miti hiyo kwa kutengeneza madari ya nyumba ya Yawe na nyumba ya kifalme, na tena kwa kutengeneza vinubi na vinanda vya waimbaji. Mpaka wakati ule miti hiyo ilikuwa haijaonekana katika inchi ya Yuda. Naye mufalme Solomono alimupatia malkia wa Seba kila kitu alichotamani, kitu chochote alichoomba zaidi ya vitu alivyomuletea mufalme. Kisha malkia akaondoka na kurudi katika inchi yake akiwa pamoja na watumishi wake. Kila mwaka, Solomono alipelekewa zahabu kadiri ya kilo elfu makumi mbili na mbili, zaidi ya zahabu aliyopokea kutoka kwa wafanya biashara na wachuuzi, tena kutoka kwa wafalme wote wa Arabia na watawala wa inchi ya Israeli. Mufalme Solomono alitengeneza ngao kubwa mia mbili; kila moja ilipakwa kadiri ya kilo saba za zahabu iliyofuliwa. Vilevile alitengeneza ngao ndogondogo mia tatu, kila moja ilipakwa zahabu yapata kilo tatu, halafu mufalme akaziweka katika jengo lililoitwa Nyumba ya Pori la Lebanoni. Tena mufalme alitengeneza kiti cha kifalme kikubwa cha pembe, na akakipakaa zahabu safi. Kiti hicho kilikuwa na ngazi sita na kiti cha kuegemea miguu cha zahabu, vyote hivyo vilikuwa vimeshikamanishwa na kiti hicho cha kifalme; na kila upande kilikuwa na pahali pa kuegemeza mikono tena kilikuwa na sanamu mbili za simba karibu na pahali pale pa kuegemeza mikono. Palikuwa sanamu kumi na mbili za simba waliosimama kwa mwisho wa kila ngazi. Kiti kama hicho kilikuwa bado kutengenezwa katika ufalme wowote. Vikombe vyote vya mufalme Solomono vilikuwa vya zahabu, na vyombo vyote vilivyokuwa katika Nyumba ya Pori ya Lebanoni vilikuwa vya zahabu safi. Feza haikuhesabiwa kuwa kitu cha bei kali katika siku za Solomono. Solomono alikuwa na mashua zilizosafiri mpaka Tarsisi na watumishi wa Hiramu, na kisha kila miaka mitatu, mashua zile zilirudi zikimuletea zahabu, feza, pembe, kima na ndege wanaoitwa tausi. Hivyo basi, mufalme Solomono aliwapita wafalme wote katika dunia kwa mali na kwa hekima. Nao wafalme wa inchi zote walikuwa na hamu ya kumwendea Solomono kwa kusikiliza hekima yake ambayo Mungu alikuwa amemujalia. Kila mumoja wao alimuletea zawadi, vyombo vya feza na vya zahabu, nguo na silaha marasi, farasi na nyumbu. Zawadi hizi alizipokea kila mwaka. Mufalme Solomono akakuwa na vibanda elfu ine vya kuwekea farasi na magari, na waaskari wapanda-farasi elfu kumi na mbili ambao aliwaweka katika miji yenye vituo vya magari ya farasi na kwake katika Yerusalema. Aliwatawala wafalme wote waliokuwa kuanzia muto Furati, mpaka inchi ya Wafilistini na mpaka kwenye mupaka na Misri. Basi Solomono alifanya feza katika Yerusalema kuwa kitu cha kawaida kama mawe katika Yerusalema, na mbao za mierezi zilipatikana kwa wingi kama mikuyu inayokuwa Sefela. Solomono aliletewa farasi walionunuliwa kutoka Misri na katika inchi zingine. Matendo mengine ya Solomono, kutoka mwanzo mpaka mwisho, yameandikwa katika kitabu cha “Historia ya Nabii Natani,” katika “Unabii wa Ahiya wa Shilo,” na katika “Maono ya Ido Mwonaji,” juu ya Yeroboamu mwana wa Nebati. Solomono alitawala inchi yote ya Israeli kwa miaka makumi ine. Kisha Solomono akakufa na kuzikwa katika muji wa baba yake Daudi. Mwana wake Rehoboamu akatawala kwa pahali pake. Basi, Rehoboamu akaenda Sekemu, ambako Waisraeli wote walikuwa wamekusanyika kwa kumuweka kuwa mufalme. Naye Yeroboamu mwana wa Nebati alipopata habari juu ya tendo hilo, wakati ule alikuwa angali anaishi Misri alikokwenda alipomukimbia Solomono, alirudi kutoka Misri. Lakini Waisraeli walituma ujumbe na kumwita. Kisha, yeye pamoja na Waisraeli wote walimwendea Rehoboamu na kumwambia: “Baba yako alitubebesha muzigo muzito. Basi, utupunguzie muzigo ule, nasi tutakutumikia.” Rehoboamu akawajibu: “Mwende murudie kwangu nyuma ya siku tatu.” Basi wakaondoka. Nyuma, Rehoboamu akataka kujua maoni ya wazee ambao walikuwa washauri wa baba yake Solomono alipokuwa angali muzima, akawauliza: “Munanishauria kwamba niwape jibu gani watu hawa?” Wazee wale wakamujibu: “Ukiwahurumia watu hawa, ukiwafurahisha na kusema nao maneno mazuri, pale watakuwa watumishi wako siku zote.” Lakini Rehoboamu alizarau shauri la wazee na kwa pahali pake akashauriana na vijana waliokomaa pamoja naye ambao walikuwa washauri wake. Basi, akawauliza: “Ninyi munatoa shauri gani kusudi tuweze kuwajibu watu hawa walioniambia: ‘Punguza muzigo ambao baba yako alitubebesha?’ ” Wale vijana wakamujibu: “Watu waliokuambia ‘Baba yako alitubebesha muzigo muzito, lakini wewe utupunguzie’, wewe uwaambie hivi: ‘Kidole changu kidogo cha mwisho ni kinene zaidi kuliko kiuno cha baba yangu. Muzigo wa baba yangu ulikuwa muzito, lakini wangu utakuwa muzito zaidi. Baba yangu aliwapiga kwa mijeledi, lakini mimi nitawapiga kwa mijeledi yenye miiba.’ ” Basi katika siku ya tatu Yeroboamu pamoja na watu wote wakarudi kwa Rehoboamu kama vile alivyokuwa amewaagiza. Naye mufalme Rehoboamu akawajibu kwa ukali, akazarau shauri la wazee, na kufuata shauri la vijana wenzake. Basi akasema: “Baba yangu aliwabebesha muzigo muzito, lakini mimi nitaufanya kuwa muzito zaidi. Baba yangu aliwapiga kwa mijeledi, lakini mimi nitawapiga kwa mijeledi yenye miiba” Halafu mufalme hakuwajali watu kwa sababu jambo hili lilisababishwa na Mungu kusudi Yawe atimize neno lake alilomwambia Yeroboamu, mwana wa Nebati kwa njia ya Ahiya wa Shilo. Lakini watu wote wa Israeli walipoona kwamba mufalme hakuwajali walimwambia: “Hatuna ushirika na Daudi! Hatuna urizi kutoka kwa mwana wa Yese. Kila mumoja arudie kwake, enyi watu wa Israeli! Utunze nyumba yako mwenyewe, ee Daudi!” Hivyo Waisraeli wote wakarudi kila mutu kwake. Lakini Rehoboamu alitawala watu wa Israeli waliokaa katika miji ya Yuda. Kisha mufalme Rehoboamu akamutuma Hadoramu aliyekuwa musimamizi wa kazi za kulazimishwa, nao watu wa Israeli walimupiga mawe, wakamwua. Halafu Rehoboamu akapanda ndani ya gari lake haraka akakimbilia Yerusalema. Hivyo, watu wa Israeli wakakuwa katika hali ya uasi juu ya utawala wa ukoo wa Daudi mpaka leo. Rehoboamu alipofika Yerusalema, alikusanya waaskari wafundi wa vita elfu mia moja na makumi nane wa makabila ya Yuda na Benjamina, apate kupigana na utawala wa Israeli, kusudi aurudishe utawala kwake yeye mwenyewe Rehoboamu. Lakini neno la Yawe lilimufikia Semaya, yule mutu wa Mungu, kusema hivi: “Umwambie Rehoboamu mwana wa Solomono, mufalme wa Yuda na Waisraeli wote katika Yuda na Benjamina kwamba Bwana anasema hivi: ‘Musiende wala musipigane na wandugu zenu. Murudie kila mutu kwake, maana yale yaliyotokea ni kwa kufuata mupango wangu.’ ” Basi wakatii ujumbe wa Yawe, wakarudia kila mutu kwake, wala hawakwenda kupigana na Yeroboamu. Rehoboamu alikaa Yerusalema na akajenga kuta kwa kuimarisha miji hii iliyokuwa katika inchi ya Yuda: Betelehemu, Etamu, Tekoa, Beti-Suri, Soko, Adulamu, Gati, Maresa, Zifu, Adoraimu, Lakisi, Azeka, Zora, Ayaloni na Hebroni. Miji hiyo yenye kuzungukwa kuta iko Yuda na Benjamina. Aliziimarisha kuta zile na mule ndani akaweka majemadari na magala ya vyakula, mafuta na divai. Ndani ya kila muji, aliweka ngao na mikuki, na kuifanya miji hiyo kuwa imara sana. Yuda na Benjamina zikakuwa chini ya mamlaka yake. Makuhani na Walawi wote waliokuwa wanaishi kote katika inchi ya Israeli, wote wakavuka mupaka wao na kumwendea. Walawi wakaacha mashamba yao ya malisho ya nyama, na maeneo yao mengine kwa sababu Yeroboamu na wana wake waliwakataza kumutumikia Yawe kama vile makuhani wa Yawe. Yeroboamu akajichagulia makuhani wake mwenyewe wa kutumika kwenye nafasi za ibada za miungu na wa kuabudu mizimu na sanamu za wana-ngombe alizojitengenezea. Watu wote ambao walikuwa wamekusudia kwa moyo kumwabudu Yawe, Mungu wa Israeli, kutoka katika makabila yote ya Israeli, waliandamana na Walawi mpaka Yerusalema kusudi wapate kumutolea sadaka Yawe, Mungu wa babu zao. Hivyo, wakaimarisha ufalme wa Yuda, na kwa muda wa miaka mitatu, wakauunga mukono utawala wa Rehoboamu mwana wa Solomono, ukakuwa imara na wakaishi katika hali ileile waliyoishi wakati walipokuwa chini ya utawala wa mufalme Daudi na mufalme Solomono. Rehoboamu alioa muke, jina lake Mahalati binti ya Yeremoti mwana wa Daudi. Mama yake aliitwa Abihaili binti ya Eliabu, mwana wa Yese. Naye akamuzalia wana watatu: Yeusi, Semaria na Zahamu. Kisha, akamwoa Maka binti ya Abusaloma, naye akamuzalia Abiya, Atai, Siza na Selomiti. Rehoboamu alioa wake kumi na wanane na wahabara makumi sita, akazaa wana makumi mbili na wane na wabinti makumi sita. Kati ya wake zake wote na wahabara wake, alimupenda zaidi Maka binti ya Abusaloma. Hivyo akamuchagua Abiya, mwana wa Maka, kuwa mukubwa kati ya wandugu zake, maana alikusudia kumufanya kuwa mufalme. Rehoboamu alifanya jambo la hekima, akawatawanya wamoja kati ya wana wake katika inchi yote ya Yuda na Benjamina akiwaweka katika miji yote yenye kuzungukwa na kuta. Wakiwa mule, akawapa vyakula vingi na vilevile akawaoea wake wengi. Wakati Rehoboamu alipoimarisha utawala wake, yeye pamoja na watu wake wote waliacha kutii Sheria ya Yawe. Katika mwaka wa tano wa utawala wake, kwa sababu hawakumutii Yawe, Sisaki, mufalme wa Misri akashambulia muji wa Yerusalema, akiwa na magari elfu moja na mia mbili, waaskari wapanda-farasi elfu makumi sita. Alikuwa vilevile na waaskari wengi sana wasioweza kuhesabiwa toka Misri; Walibia, Wasuki na Waetiopia. Aliteka miji yenye kuzungukwa na kuta katika Yuda, akafika mpaka Yerusalema. Kisha Nabii Semaya akamwendea mufalme Rehoboamu na wakubwa wa Yuda, waliokusanyika Yerusalema ambapo walikimbilia kwa kumwepuka Sisaki, akamwambia: “Yawe anasema hivi: ‘Ninyi mumeniacha mimi, kwa hiyo basi, nami nimewaacha ninyi na kuwatia katika mikono ya Sisaki.’ ” Halafu wakubwa wa Israeli na mufalme wakajinyenyekeza, wakasema: “Yawe ni mwenye haki.” Yawe alipoona kwamba wamejinyenyekeza, akazungumuza tena na nabii Semaya, akamwambia: “Wamejinyenyekeza, sitawaangamiza, lakini nitawaokoa nyuma ya muda mufupi. Sitashushia muji Yerusalema kasirani yangu na kuuharibu kwa mukono wa Sisaki, lakini watamutumikia kusudi wapate kujua tofauti inayokuwa kati ya kunitumikia mimi na kuwatumikia wafalme wa dunia.” Basi, mufalme Sisaki wa Misri akashambulia muji Yerusalema, akaichukua hazina yote ya nyumba ya Yawe na ya nyumba ya kifalme, pamoja na ngao za zahabu ambazo mufalme Solomono alizozitengeneza. Kwa pahali pa ngao hizo, mufalme Rehoboamu akatengeneza ngao za shaba na kuziweka chini ya ulinzi wa walinzi wa mulango wa nyumba ya kifalme. Kila wakati mufalme alipokwenda katika nyumba ya Yawe, walinzi waliingia walibeba ngao zile na kisha walizirudisha katika chumba cha ulinzi. Alipojinyenyekeza, Yawe akaacha kumukasirikia na hakumwangamiza kabisa. Zaidi ya hayo, hali ya inchi ya Yuda ilikuwa nzuri. Basi mufalme Rehoboamu akajiimarisha zaidi katika Yerusalema, na kutawala Yuda. Alikuwa na umri wa miaka makumi ine na mumoja alipoanza kutawala. Naye alitawala kwa muda wa miaka kumi na saba katika Yerusalema, muji ambao Yawe aliuchagua kati ya makabila yote ya Israeli kusudi aabudiwe ndani yake. Mama ya Rehoboamu aliitwa Nama, kutoka Amoni. Rehoboamu alitenda maovu, kwa maana hakutayarisha moyo wake kwa kumutafuta Yawe. Matendo ya mufalme Rehoboamu tangu mwanzo mpaka ya mwisho yameandikwa katika kitabu cha “Mambo ya Siku ya nabii Semaya”, na “Mambo ya Siku ya nabii Ido.” Wakati huu wote, kulikuwa vita ya mufululizo kati ya Rehoboamu na Yeroboamu. Kisha Rehoboamu alikufa na kuzikwa katika muji wa Daudi, na Abiya mwana wake akatawala kwa pahali pake. Abiya akaanza kutawala inchi ya Yuda katika mwaka wa kumi na nane wa utawala wa mufalme Yeroboamu. Alitawala kwa muda wa miaka mitatu akiwa Yerusalema. Mama yake aliitwa Mikaya binti ya Urieli wa Gibea. Kukatokea vita kati ya Abiya na Yeroboamu. Abiya alijitayarisha kupigana vita akiwa na jeshi la waaskari hodari elfu mia ine, naye Yeroboamu akajitayarisha na jeshi lake la waaskari hodari elfu mia nane. Mufalme Abiya akasimama juu ya mulima Zemaraimu, unaokuwa kati ya milima ya Efuraimu akamwambia Yeroboamu na Waisraeli: “Unisikilize, ewe Yeroboamu na Waisraeli wote! Hamujui kwamba Yawe, Mungu wa Israeli, amemupa Daudi na wazao wake ufalme kwa milele kwa kufanya naye agano lisilovunjika? Lakini Yeroboamu mwana wa Nebati mutumishi wa Solomono mwana wa Daudi alimwasi bwana wake. Na watu wa ovyoovyo wakajiunga naye, watu wapumbafu wasiofaa kitu, nao wakamushawishi Rehoboamu mwana wa Solomono kutenda yale waliyotaka wao, naye hangeweza kuwazuia maana wakati ule alikuwa angali kijana bila mazoezi mengi. “Sasa ninyi munazani munaweza kupinga ufalme wa Yawe ambao Daudi na wazao wake walipewa kwa sababu muko na jeshi kubwa na sanamu za zahabu za wana-ngombe, Yeroboamu alizowatengenezea kuwa miungu yenu! Hamukuwafukuza makuhani wa Yawe, wana wa Haruni, vilevile na Walawi, na kujifanyia makuhani wenu wenyewe kama vile watu wa mataifa mengine wanavyofanya? Yeyote anayekuja kwenu kujitakasa na mwana-ngombe dume au kondoo dume anakuwa kuhani wa vitu ambavyo si miungu. “Lakini kwa ngambo yetu, Yawe ni Mungu wetu, wala hatujamwacha. Tena tuko na makuhani wa uzao wa Haruni ambao wanamutumikia Yawe, nao wanasaidiwa na Walawi. Kila siku asubui na magaribi, makuhani wanamutolea sadaka za kuteketezwa na kumufukizia ubani wenye harufu nzuri, tena wanapanga mikate inayotolewa na Mungu juu ya meza ya zahabu safi, na kutunza kinara cha zahabu na kuwasha taa kila siku magaribi. Sisi tunayafuata maagizo ya Yawe, Mungu wetu, lakini ninyi mumemwacha. Na muangalie, Mungu mwenyewe ndiye kiongozi wetu na makuhani wake wako na baragumu zao tayari kuzipiga kwa kupana kitambulisho cha kuanza vita juu yenu. Enyi watu wa Israeli, muache kupigana vita na Yawe, Mungu wa babu zenu. Hamuwezi kushinda!” Lakini wakati ule, Yeroboamu alikuwa amekwisha kutuma waaskari wake wamoja kushambulia jeshi la Yuda kutoka upande wa nyuma, wakati wale wengine wamewashambulia kutoka upande wa mbele. Watu wa Yuda walipoangalia nyuma, walishituka kuona wamezungukwa; basi wakamulilia Yawe, nao makuhani wakapiga baragumu zao. Halafu waaskari wa Yuda wakapiga kelele la vita, na walipofanya hivyo, Mungu akamushinda Yeroboamu na jeshi lake la Waisraeli mbele ya Abiya na watu wa Yuda. Watu wa Israeli wakawakimbia Wayuda naye Mungu akawatia katika mikono yao. Abiya na jeshi lake akawapiga Waisraeli sana, akawashinda; akaua waaskari wa Israeli, elfu mia tano waliokuwa kati ya waaskari hodari sana katika Israeli. Kwa hiyo, watu wa Yuda walipata ushindi mbele ya Waisraeli kwa sababu walimutegemea Yawe, Mungu wa babu zao. Abiya akamufukuza Yeroboamu, akamunyanganya miji yake: Beteli, Yesana, Efuroni pamoja na vijiji vilivyokuwa kandokando ya miji hiyo. Yeroboamu hakuweza kupata nguvu tena wakati wa Abiya. Kwa mwisho Yawe akamupiga, naye akakufa. Lakini Abiya aliendelea kupata nguvu zaidi. Akaoa wanawake kumi na wane, akazaa wana makumi mbili na wawili na wabinti kumi na sita. Matendo mengine ya Abiya, njia zake na maneno yake, yameandikwa katika kitabu cha “Historia ya Nabii Ido.” Kwa mwisho, Abiya alikufa na kuzikwa katika muji wa Daudi na mwana wake Asa akatawala kwa pahali pake. Wakati wa Asa, kulikuwa amani katika inchi kwa muda wa miaka kumi. Asa akatenda mambo yanayokuwa mazuri na sawa mbele ya Yawe, Mungu wake. Aliondoa katika inchi mazabahu za kigeni na pahali pa kuabudia miungu mingine, akabomoa minara na kukatakata sanamu za Ashera. Aliwaamuru watu wa Yuda wamutafute Yawe, Mungu wa babu zao, na kutii Sheria na amri. Vilevile aliondoa pahali pote pa kuabudia miungu mingine na meza za kufukizia ubani kutoka katika miji yote ya Yuda; halafu ufalme wake ulikuwa na amani chini ya utawala wake. Alijenga miji yenye kuta za kuiimarisha inchi ya Yuda wakati ule wa amani, na kwa muda wa miaka ile, hapakutokea vita kwa maana Yawe alimupa amani. Naye Asa akawaambia watu wa Yuda: “Tujenge miji hii na kuizungushia kuta na minara, milango yenye vifungio vya vyuma. Inchi ingali katika mikono yetu kwa maana tumetenda mapenzi ya Yawe, Mungu wetu, naye ametupatia amani pande zote.” Basi wakajenga na kufanikiwa. Mufalme Asa alikuwa na jeshi la waaskari elfu mia tatu kutoka Yuda, wenye ngao na mikuki, na wengine elfu mia mbili na makumi nane kutoka katika kabila la Benjamina, wenye ngao na pinde. Wote walikuwa watu mashujaa sana. Zera, Mwetiopia alishambulia inchi ya Yuda akiwa na jeshi la waaskari milioni moja na magari mia tatu, akasonga mbele mpaka Maresa. Asa alitoka akaenda kupigana naye. Pande zote mbili zilijipanga katika Bonde la Sefata karibu na Maresa. Hapo Asa akamulilia Yawe, Mungu wake, akisema: “Ee Yawe, hakuna mwingine kama wewe, mwenye uwezo wa kusaidia jeshi likuwe zaifu au lenye nguvu. Utusaidie, ee Yawe, Mungu wetu, kwa sababu sisi tunakutegemea wewe, na kwa jina lako tumekuja kupigana vita na jeshi hili kubwa ajabu. Ee Yawe, wewe ndiwe Mungu wetu; usimuruhusu mwanadamu yeyote ashindane nawe.” Yawe akawashinda Waetiopia mbele ya Asa na jeshi lake la watu wa Yuda. Waetiopia wakakimbia. Asa pamoja na waaskari wake wakawafuatilia mpaka Gerari, wakawaua Waetiopia wengi sana, hapakubaki hata mumoja, maana walikuwa wamekwisha kushindwa na Yawe pamoja na jeshi lake. Jeshi la Yuda likateka vitu vingi sana. Likaharibu miji yote iliyokuwa kandokando ya Gerari, kwa kuwa watu waliokuwa katika miji ile, walipatwa na hofu ya Yawe. Likabeba mali nyingi kutoka katika miji ile, kwa sababu kulikuwa mali mengi sana. Likashambulia vilevile wachungaji, likachukua kondoo wengi na ngamia. Kisha likarudia Yerusalema. Roho wa Mungu alimujaza Azaria mwana wa Obedi, naye akatoka kwenda kukutana na mufalme Asa, akamwambia: “Unisikilize, ee Asa na watu wote wa kabila la Yuda na la Benjamina! Yawe yuko pamoja nanyi, ikiwa mutakuwa pamoja naye. Mukimutafuta, mutamupata, lakini mukimwacha, naye atawaacha. Kwa muda murefu sasa, Waisraeli wameishi bila Mungu wa kweli, wala makuhani wa kuwafundisha, na bila Sheria. Lakini walipopatwa na shida, walimugeukia Yawe, Mungu wa Israeli, wakamutafuta, wakamupata. Katika siku zile, hakuna mutu aliyeweza kuingia wala kutoka kwa usalama kwa sababu hapakukuwa amani; fujo nyingi sana ziliwasumbua wanainchi wa kila inchi. Taifa moja lilipigana na taifa lingine na muji mumoja ulipigana na muji mwingine, kwa sababu Mungu aliwafazaisha kwa taabu za kila aina. Lakini ninyi mujipe moyo, wala musiregee kwa maana mutapata malipo kwa kazi munayofanya.” Asa aliposikia maneno haya, ni kusema unabii wa Azaria mwana wa Odedi, yakamutia moyo. Akaondoa sanamu zote za kuchukiza katika inchi yote ya Yuda na ya Benjamina, na kutoka katika miji yote aliyoteka katika inchi ya milima ya Efuraimu. Na kisha akatengeneza upya mazabahu ya Yawe iliyokuwa katika baraza la nyumba ya Yawe. Asa akakusanya watu wote wa Yuda na Benjamina, na wengine wote waliokuwa wakikaa katika inchi yake kutoka kabila la Efuraimu, la Manase na la Simeoni. Hawa walikuja kwake walipoona kwamba Yawe, Mungu wake yuko pamoja naye. Wote walikusanyika Yerusalema katika mwezi wa tatu wa mwaka wa kumi na tano wa utawala wa Asa. Siku ile, walimutolea Yawe sadaka za ngombe mia saba na kondoo elfu saba, kutoka katika vile vitu walivyoteka. Nao wakafanya agano, kwamba watamutafuta Yawe, Mungu wa babu zao, kwa moyo wote na kwa roho yao yote; na kwamba yeyote asiyemutafuta Yawe, Mungu wa Israeli, akuwe kijana au muzee, mwanaume au mwanamuke, sharti auawe. Walimwapia Yawe kwa sauti kubwa, wakalalamika zaidi, wakapiga ngunga na baragumu. Watu wote wa Yuda walikuwa na furaha tele kwa sababu walikuwa wameapa kwa moyo wote. Walikuwa wamemutafuta kwa hamu, wakamupata. Naye Yawe akawapa amani pande zote. Mufalme Asa alimwondoa hata mama yake Maka, cheo chake cha malkia, kwa sababu alitengeneza sanamu ya kuchukiza ya Ashera, mungu wa kike. Asa alikatakata sanamu hiyo, akaipondaponda na kuiteketeza kwa moto katika bonde la kijito Kidroni. Lakini hata hivyo pahali pa kutambikia miungu mingine katika Israeli hapakuharibiwa; lakini yeye alikuwa na moyo mwaminifu maisha yake yote. Alivirudisha katika nyumba ya Mungu vifaa vyote vilivyotakaswa na baba yake pamoja na vile alivyotakasa yeye mwenyewe; feza na zahabu na vyombo vingine. Hapakukuwa vita tena katika inchi mpaka mwaka wa makumi tatu na tano wa utawala wa Asa. Katika mwaka wa makumi tatu na sita wa utawala wa mufalme Asa, Basha, mufalme wa Israeli, alishambulia inchi ya Yuda na kuanza kujenga muji wa Rama kusudi apate kuzuia mutu yeyote asitoke wala asiingie kwa Asa, mufalme wa Yuda. Kwa hiyo mufalme Asa akatwaa feza na zahabu kutoka katika hazina ya nyumba ya Yawe na ya nyumba ya kifalme, akazituma Damasiki kwa Beni-Hadadi, mufalme wa Suria, na ujumbe akasema: “Tufanye mapatano ya ushirikiano kati yangu na wewe kama vile baba yangu na baba yako walivyofanya. Angalia ninakutumia zawadi ya feza na zahabu, kwenda uvunje mapatano ya ushirikiano unaokuwa kati yako na mufalme Basha wa Israeli kusudi aache mashambulizi juu yangu.” Hapo mufalme Beni-Hadadi akakubali pendekezo la mufalme Asa. Akawatuma majemadari wake na majeshi yake kwenda kushambulia miji ya Israeli. Nao wakateka miji ya Iyoni, Dani, Abeli-Maimu, na miji yote ya Nafutali iliyokuwa na hazina. Mufalme Basha alipopata habari za mashambulizi hayo, akaacha kujenga muji wa Rama, akasimamisha kazi yake. Kisha mufalme Asa aliwapeleka watu wote wa inchi ya Yuda, wakahamisha mawe ya Rama na mbao, vifaa ambavyo Basha alitumia kwa kujenga. Kisha Asa akatumia vifaa hivyo kwa kujenga miji ya Geba na Misipa. Kwa wakati ule, nabii Hanani akamwendea mufalme Asa wa Yuda, akamwambia: “Kwa sababu ulimutegemea mufalme wa Suria kuliko kumutegemea Yawe, Mungu wako, jeshi la mufalme wa Suria limekuponyoka. Wale Waetiopia na Walibia hawakukuwa jeshi kubwa na magari na waaskari wapanda-farasi wengi? Lakini kwa vile ulimutegemea Yawe, yeye aliwatia katika mikono yako. Yawe anachunga kwa uangalifu ulimwengu wote, kwa kuwapa nguvu wale wanaokuwa waaminifu kwake. Umetenda jambo la kipumbafu, kwa hiyo tangu sasa, utakuwa na vita kila mara.” Kwa hiyo, Asa akamukasirikia sana nabii Hanani, hata akamuweka katika kifungo; maana amekuwa na hasira kubwa naye juu ya maneno yale. Wakati uleule, Asa akaanza kuwatesa vikali wamoja kati ya watu. Matendo ya Asa, toka mwanzo mpaka mwisho, yameandikwa katika Kitabu cha Wafalme wa Yuda na Israeli. Katika mwaka wa makumi tatu na kenda wa utawala wake, Asa akashikwa na ugonjwa wa miguu. Ugonjwa ule ukazidi sana kuongezeka. Lakini hata wakati ule, Asa hakumugeukia Yawe amusaidie, lakini alijitafutia musaada kutoka kwa waganga. Asa akakufa katika mwaka wa makumi ine na moja wa utawala wake. Akazikwa katika kaburi alilokuwa amejichimbia yeye mwenyewe, katika muji wa Daudi. Walimulalisha juu ya kitanda kilichokuwa kimejazwa marasi ya kila aina yaliyotayarishwa na wafundi wa kutengeneza marasi, wakawasha moto mukubwa sana kwa heshima yake. Naye Yosafati mwana wake akatawala pahali pa baba yake Asa, akajiimarisha juu ya inchi ya Israeli. Aliweka majeshi katika miji yote ya inchi ya Yuda yenye kuta, na katika maeneo mengine ya Yuda akaweka waaskari walinzi, na katika miji ya Efuraimu ambayo baba yake Asa aliiteka. Yawe alikuwa pamoja na Yosafati kwa sababu alifuata njia za kwanza za babu yake Daudi, wala hakumwabudu mungu Bali. Yeye alimutafuta Mungu wa babu yake na kutii amri zake, wala hakufuata matendo ya Israeli. Yawe, akauimarisha ufalme wa Yuda katika mikono ya Yosafati, nao watu wote wakamuletea zawadi, akatajirika sana na kuheshimika. Alipenda sana ndani ya moyo kumutumikia Yawe, na zaidi ya hayo, alipaharibu pahali pote pa kuabudia miungu mingine na sanamu za Ashera, mungu wa kike, katika inchi ya Yuda. Katika mwaka wa tatu wa utawala wake, Yosafati akawatuma wakubwa hawa wafundishe katika miji ya Yuda: Ben-Haili, Obadia, Zakaria, Netaneli na Mikaya. Walawi kenda na Makuhani wawili wakaandamana nao. Walawi hao walikuwa Semaya, Netania, Zebadia, Asaeli, Semiramoti, Yonatani, Adonia, Tobia na Tobu-Adonia; nao makuhani walikuwa Elisama na Yoramu. Walitwaa kitabu cha Sheria ya Yawe, wakazunguka nacho katika miji yote ya Yuda wakifundisha watu. Yawe akaogopesha falme zote jirani za inchi ya Yuda, zikaogopa kupigana vita na Yosafati. Vilevile Wafilistini wamoja wakamuletea Yosafati zawadi pamoja na feza nyingi na Waarabu wengine nao wakamuletea kondoo dume elfu saba na mia saba, na mbuzi dume elfu saba na mia saba. Kwa hiyo Yosafati akaendelea kuwa mukubwa zaidi. Akajenga makimbilio na miji ya hazina. Naye alikuwa na hazina kubwa katika miji ya Yuda. Kule Yerusalema, aliweka waaskari wa jeshi mashujaa. Hii ndiyo hesabu yao kulingana na ukoo za babu zao: Adina alikuwa jemadari wa vikundi vya waaskari elfu wa kabila la Yuda. Chini yake, kulikuwa waaskari elfu mia tatu. Wa pili nyuma yake katika cheo alikuwa jemadari Yohanani, akiwa na waaskari elfu mia mbili na makumi nane, na wa tatu alikuwa Amasia mwana wa Sikiri, akiwa na waaskari mashujaa elfu mia mbili. Amasia alijitolea kwa mapenzi yake kumutumikia Yawe. Jemadari wa vikundi vya waaskari waliotoka katika kabila la Benjamina alikuwa Eliada, mutu hodari, naye alikuwa na waaskari elfu mia mbili, wenye pinde na ngao. Wa pili nyuma yake alikuwa Yozabadi, aliyekuwa na waaskari elfu mia moja makumi nane waliojitayarisha kwa vita. Watu wote hao walimutumikia mufalme kule Yerusalema, na zaidi ya hayo, aliweka waaskari wengine katika miji ile mingine yenye makimbilio kote katika inchi ya Yuda. Wakati mufalme Yosafati wa Yuda alipokuwa amekwisha kuwa mutu tajiri na mwenye heshima, alifanya mupango wa ndoa kati ya jamaa yake, na jamaa ya mufalme Ahabu wa Israeli. Nyuma ya miaka fulani Yosafati akakwenda Samaria kumutembelea mufalme Ahabu. Ahabu akamuchinjia Yosafati kondoo na ngombe wengi, kwa heshima yake pamoja na watu waliokuwa pamoja naye, kisha akamushawishi aende pamoja naye kwa kushambulia muji wa Ramoti-Gileadi. Ahabu mufalme wa Israeli akamwambia Yosafati mufalme wa Yuda: “Utakwenda pamoja nami kwa kushambulia muji wa Ramoti-Gileadi?” Naye akajibu: “Mimi niko kama wewe, na watu wangu ni kama watu wako. Tutakuwa pamoja nawe katika vita.” Kisha Yosafati akaendelea kumwambia mufalme wa Israeli: “Lakini ninakusihi uombe kwanza shauri la Yawe.” Basi Ahabu akakusanya manabii mia ine, akawauliza: “Twende kushambulia muji wa Ramoti-Gileadi, au nisiende?” Wakamujibu: “Kwenda! Mungu atakupatia ushindi!” Lakini, Yosafati akauliza: “Hapa hakuna nabii mwingine wa Yawe ambaye tunaweza kumwuliza shauri?” Naye mufalme wa Israeli akamujibu Yosafati: “Kungali mumoja, Mikaya mwana wa Imula. Yeye tunaweza kumwuliza shauri la Yawe. Lakini ninamuchukia sana kwa sababu yeye hatabiri jambo jema juu yangu hata kidogo, lakini mabaya tu.” Yosafati akamwambia: “Si vizuri kwa mufalme kusema hivyo.” Basi, Ahabu, mufalme wa Israeli akamwita mukubwa mumoja na kumwamuru: “Haraka, kwenda umulete Mikaya mwana wa Imula.” Wakati ule, mufalme wa Israeli pamoja na Yosafati, mufalme wa Yuda, walikuwa wameikaa katika viti vyao vya kifalme kwenye kiwanja cha kupepetea ngano kwenye mulango wa kuingilia muji wa Samaria nao walikuwa wakivaa nguo zao za kifalme. Wakati ule manabii wote walikuwa wakitoa unabii wao mbele yao. Kisha mumoja wa manabii wale, Zedekia mwana wa Kenana, akajitengenezea pembe za chuma na kusema: “Yawe anasema hivi: ‘Kwa pembe hizi, utawarudisha nyuma Wasuria hata kuwaangamiza.’ ” Na wale manabii wengine wakatabiri vile vile wakasema: “Kwenda kushambulia muji wa Ramoti-Gileadi na kufanikiwa. Yawe atautia katika mikono yako.” Wakati ule, yule mutumishi aliyetumwa kwa Mikaya akamwambia: “Manabii wengine wote kwa pamoja wamemutabiria mufalme ushindi; tafazali nawe vilevile ufanye kama wao umutabirie mazuri.” Lakini Mikaya akamujibu: “Kama vile Yawe anavyoishi, kile Mungu wangu atakachoniambia, ndicho nitakachosema.” Basi Mikaya alipofika mbele ya mufalme, mufalme akamwuliza: “Twende kupigana vita kule Ramoti-Gileadi au nisiende?” Mikaya akajibu: “Kwenda na ufanikiwe, naye Yawe atawatia katika mikono yako.” Lakini mufalme akamwambia: “Nitakuapisha mara ngapi kwamba kila mara unaposema nami kwa jina la Yawe, unapaswa kuniambia ukweli?” Naye Mikaya akasema: “Niliwaona watu wote wa Israeli wakitawanyika juu ya milima kama kondoo wasiokuwa na muchungaji. Naye Yawe akasema: ‘Watu hawa hawana kiongozi; uwaache warudi kila mutu kwake kwa amani.’ ” Halafu mufalme wa Israeli akamwambia Yosafati: “Sikukuambia kwamba hatatabiri jema juu yangu, lakini mabaya tu?” Kisha Mikaya akasema: “Basi sikia neno la Yawe: Nilimwona Yawe akikaa katika kiti chake cha kifalme na jeshi lake lote la mbinguni likisimama upande wake wa kuume na wa kushoto. Halafu Yawe akauliza: ‘Ni nani atakayemushawishi Ahabu mufalme wa Israeli aende aangamie kule Ramoti-Gileadi?’ Kila mumoja akajibu sawa alivyofikiri. Kisha, pepo mumoja akajitokeza mbele ya Yawe, akasema: ‘Mimi nitamushawishi.’ Yawe akamwuliza: ‘Kwa njia gani?’ Naye akajibu: ‘Nitakwenda na kuwasukuma manabii wake wote waseme uongo.’ Yawe akamwambia: ‘Wewe utamushawishi na utashinda; kwenda kufanya hivyo.’ “Basi sasa angalia: Yawe ametia pepo wa uongo katika vinywa vya manabii wako. Lakini Yawe amesema mabaya juu yako!” Kisha nabii Zedekia mwana wa Kenana akamukaribia Mikaya, akamupiga kofi kwenye shavu na kumwuliza: “Kwa njia gani Roho wa Yawe ameniacha na akakuja kusema nawe?” Mikaya akamujibu: “Utatambua mambo haya siku ile utakapoingia katika chumba cha ndani kwa kujificha.” Naye mufalme wa Israeli akatoa amri: “Mumukamate Mikaya mumurudishe kwa Amoni, liwali wa muji, na kwa Yoasi, mwana wa mufalme, na kusema: ‘Mufalme anasema hivi: Mumuweke mutu huyu katika kifungo na kumulisha kwa mukate kidogo na maji kidogo, mpaka nitakaporudi salama.’ ” Mikaya akasema: “Ukirudi salama, basi, utajua kwamba Yawe hakusema nami.” Kisha akaendelea kusema: “Musikie, enyi watu wote!” Basi, mufalme wa Israeli akaenda pamoja na Yosafati mufalme wa Yuda kwa kuushambulia muji wa Ramoti-Gileadi. Mufalme wa Israeli akamwambia Yosafati: “Mimi nitavaa nguo zisizokuwa za kifalme kwa kuingia katika vita, lakini wewe utavaa nguo yako ya kifalme.” Hivyo mufalme wa Israeli akaenda kwa vita bila kuvaa nguo za kifalme. Mufalme wa Suria alikuwa amewaamuru wakubwa wa waaskari wake waliosimamia magari yake ya vita akisema: “Musipigane na mutu ye yote mukubwa au mudogo, lakini tu na mufalme wa Israeli.” Halafu wakubwa wale walipomwona Yosafati, wakasema: “Huyu ndiye mufalme wa Israeli.” Kwa hiyo, wakamwelekea kwa kumushambulia; lakini Yosafati akapiga kelele, na Yawe akamwokoa. Mungu akawaondoa wale waliokuwa karibu kumushambulia. Wakubwa wa waaskari walipotambua kwamba hakukuwa mufalme wa Israeli, wakaacha kumushambulia, wakarudi. Lakini askari mumoja wa Suria akauvuta upinde wake, kwa kubahatisha, akamupiga mufalme wa Israeli mushale katika nafasi ya maunganio ya nguo yake ya chuma ya kujikinga kifua. Hapo Ahabu akamwambia mwongozi wa gari lake la vita: “Geuza gari uniondoe katika vita nimeumizwa.” Nayo mapigano siku ile, yakazidi kuwa makali wakati mufalme wa Israeli amejiegemeza mwenyewe ndani ya gari akiwaelekea Wasuria mpaka magaribi. Halafu wakati jua liliposhuka, akakufa. Mufalme Yosafati wa Yuda akarudi salama katika nyumba yake ya kifalme katika muji wa Yerusalema. Lakini nabii Yehu mwana wa Hanani, akakwenda kukutana na mufalme, akamwambia: “Unazani ni vema kuwasaidia waovu na kuwapenda wanaomuchukia Yawe? Mambo uliyofanya yamekuletea kasirani ya Yawe. Lakini, kuna wema fulani ndani yako. Umekwisha kuondoa sanamu zote za Ashera, mungu wa kike, na umejikaza sana kumutafuta Mungu kwa moyo wote.” Mufalme Yosafati akakaa Yerusalema, lakini hata hivyo, mara kwa mara aliwatembelea watu wa Beri-Seba upande wa kusini, mpaka kwenye milima ya Efuraimu, upande wa kaskazini. Alifanya hivyo kwa kuwavuta watu wamurudilie Yawe, Mungu wa babu zao. Akaweka waamuzi katika miji yote ya Yuda yenye kuta, akawaambia: “Muwe waangalifu sana wakati munapoamua, kwa maana hukumu munayotoa hamuitoi kwa amri ya mwanadamu, lakini kwa amri inayotoka kwa Yawe, naye yuko pamoja nanyi munapotoa uamuzi. Basi, sasa mumwogope Yawe, mukuwe waangalifu katika kila jambo mutakalotenda kwa sababu Yawe wetu hatavumilia upotoshaji wa haki, wala upendeleo wala upokeaji wa kituliro.” Katika muji wa Yerusalema, Yosafati akaweka Walawi makuhani na wakubwa wa jamaa za Waisraeli wakuwe waamuzi wa magomvi yanayoelekea sheria za Yawe, au ugomvi kati ya wakaaji wa muji. Akawaamuru akisema: “Ndivyo mutakavyotenda mukimwogopa Yawe, kwa uaminifu na kwa moyo wote. Kila mara wandugu zenu kutoka katika muji wowote wanapowaletea mashitaki yoyote juu ya uuaji, kuvunja Sheria, amri, kanuni au maagizo, muwashaurie vema kusudi wasimukosee Yawe. Musipofanya hivyo, ninyi pamoja na wandugu zenu mutapatwa na kasirani ya Yawe. Lakini mukitenda vile, hamutakuwa na kosa. Amaria, Kuhani Mukubwa, ndiye atakayesimamia mambo yote yanayoelekea Yawe, naye Zebadia mwana wa Isimaeli, musimamizi wa inchi ya Yuda atasimamia mambo yote ya utawala, na Walawi watakuwa wakubwa. Mujipe moyo mutimize masharti haya, naye Yawe akuwe pamoja nao wanaokuwa wema.” Nyuma ya mambo hayo, majeshi ya Wamoabu na Waamoni pamoja na sehemu ya Wameuni wakashambulia inchi ya Yuda. Watu wamoja wakakuja kumwambia mufalme Yosafati: “Jeshi kubwa limekuja kukushambulia kutoka Edomu, ngambo ya bahari ya Chumvi. Tayari wamekwisha kufika Hazazoni-Tamari.” (Hili ni jina lingine la Engedi). Yosafati akashikwa na woga, akamwomba Yawe amwongoze. Akatangaza kwamba watu wote katika inchi ya Yuda wafunge kula. Watu wakakuja Yerusalema kutoka miji yote ya Yuda, wakakusanyika kwa kumwomba Yawe awasaidie. Yosafati akasimama katikati ya kusanyiko la watu wa Yuda na Yerusalema mbele ya kiwanja kipya cha nyumba ya Yawe, akaomba kwa sauti akisema: “Ee Yawe, Mungu wa babu zetu, wewe ndiwe Mungu unayekuwa mbinguni! Wewe unatawala falme zote katika dunia, una uwezo na nguvu, wala hakuna anayeweza kukupinga. Si wewe, ee Mungu wetu, uliyewafukuza wenyeji wa inchi hii wakati watu wako Waisraeli walipoingia katika inchi hii, ukawapa wazao wa Abrahamu rafiki yako, ikuwe yao milele? Nao wamekaa humu, na kukujengea hekalu kwa heshima ya jina lako, wakijua kwamba wakipatwa na hasara yoyote, azabu, vita, ugonjwa mukali, au njaa, basi watakuja na kusimama mbele ya nyumba hii mbele yako, wakulilie katika shida zao, nawe utawasikiliza na kuwaokoa. Sasa Waamoni, Wamoabu na watu wa mulima Seiri, ambao haukuwaruhusu babu zetu washambulie inchi zao walipotoka Misri, wakapitia kandokando wasiwaangamize, angalia, jinsi wanavyotulipa. Wanakuja kutuondoa katika inchi yako uliyoturizisha ikuwe urizi wetu. Wewe ndiwe Mungu wetu! Uwaazibu, maana sisi hatuna uwezo wowote mbele ya jeshi kubwa kama hili linalotufikia. Hatujui la kufanya lakini tunatazamia musaada kutoka kwako.” Wanaume wote wa Yuda, pamoja na wake zao na watoto wao, walikuwa wakisimama pale mbele ya Yawe. Halafu Roho wa Yawe akamujaza Mulawi mumoja aliyekuwa pale. Jina lake Yahazieli mwana wa Zakaria, aliyekuwa mwana wa Benaya, mwana wa Yeieli, mwana wa Matania, wa ukoo wa Asafu. Yahazieli akasema: “Musikilize ninyi watu wa Yuda na wakajii wa Yerusalema na mufalme Yosafati, Yawe anawaambia hivi: musiogope wala musihangaike kwa sababu ya jeshi hili kubwa. Vita hivi si vyenu, lakini ni vya Mungu. Kesho muwashambulie wakati watakapokuwa wakipanda Bonde la Sisi. Mutawakuta mwisho wa bonde, upande wa mashariki wa jangwa la Yerueli. Hamutahitaji kupigana vita hivi. Ninyi mujipange tu halafu mungojee, na mutaona Yawe akiwashinda kwa jina lenu. Enyi watu wa Yuda na Yerusalema, musiogope wala musifazaike. Muende kwa vita, naye Yawe atakuwa pamoja nanyi!” Kisha mufalme Yosafati akainama uso mpaka chini pamoja na watu wote wa Yuda na wakaaji wa Yerusalema na kumwabudu Yawe. Walawi na ukoo wa Kohati na Kora, wakasimama na kumusifu Yawe, Mungu wa Israeli, kwa sauti kubwa sana. Kesho yake, wakaamuka asubui mapema, wakaenda mpaka katika jangwa la Tekoa. Walipokuwa wanaondoka, Yosafati akasimama, akawaambia: “Musikilize, enyi watu wa Yuda na wakaaji wa Yerusalema! Mumwamini Yawe, Mungu wenu, nanyi mutakuwa imara. Muwaaminie manabii wake, nanyi mutashinda.” Nyuma ya kushauriana na watu, mufalme akachagua waimbaji kwa kumwimbia Yawe wavae nguo zao takatifu kisha watangulie mbele ya jeshi, wakiimba: “Mumushukuru Yawe, maana wema wake unadumu milele!” Wakati walipoanza kuimba na kusifu, Yawe akawavuruga akili waaskari Waamoni, Wamoabu na watu wa mulima Seiri waliokuja kupigana na Yuda. Na waaskari wale wakashindwa. Waamoni na Wamoabu wakawashambulia wenyeji wa mulima Seiri, na kuwaangamiza kabisa. Kisha kuwaangamiza wakaaji wa mulima Seiri wakaanza kushambuliana wao kwa wao, wakaangamizana. Jeshi la Yuda lilipofika kwenye munara wa ulinzi kule katika jangwa, wakaangalia upande wa waadui, wakaona maiti zimesambaa kila pahali. Hakuna mutu yeyote aliyeponyoka. Yosafati na waaskari wake wakaenda kukamata vitu. Wakakuta ngombe wengi, mali, nguo na vitu vingine vya bei kali. Iliwachukua muda wa siku tatu kusomba vitu hivyo, na hata hivyo, hawakuvimaliza maana vilikuwa vingi sana. Siku ya ine wakakusanyika katika Bonde la Sifa, na kumusifu Yawe kwa yote aliyowafanyia. Hii ndiyo sababu bonde hilo linaitwa Bonde la Sifa mpaka hivi leo. Kisha Yosafati akawaongoza waaskari wake mpaka Yerusalema kwa shangwe, kwa sababu Yawe aliwashinda waadui zao. Walipofika Yerusalema, walikwenda moja kwa moja mpaka kwenye nyumba ya Yawe, wakipiga vinanda, vinubi na baragumu. Falme zote zikaingiwa na hofu ziliposikia jinsi Yawe alivyowashinda waadui za Israeli. Basi, Yosafati akatawala kwa amani, na Mungu akamupa amani pande zote. Yosafati alikuwa na umri wa miaka makumi tatu na mitano alipoanza kutawala inchi ya Yuda. Alitawala kutoka Yerusalema kwa muda wa miaka makumi mbili na tano. Jina la mama yake ni Azuba binti ya Silihi. Yosafati alitenda mema mbele ya Yawe kama vile Asa baba yake alivyofanya. Lakini hakuharibu pahali pa kutambikia sadaka juu ya kilima. Watu walikuwa wangali hawajamugeukia na kumwabudu Mungu wa babu zao kwa mioyo yao. Matendo mengine ya Yosafati, kutoka mwanzo wa utawala wake mpaka mwisho, yameandikwa katika Kitabu cha Mambo ya Yehu mwana wa Hanani, ambacho kiko katika Kitabu cha Wafalme wa Israeli. Nyuma ya hayo, Yosafati mufalme wa Yuda, akajiunga na Ahazia mufalme wa Israeli, aliyetenda mambo maovu. Walishirikiana kutengeneza mashua za kusafiri mpaka Tarsisi, walizitengenezea kule Esioni-Geberi. Lakini Eliezeri mwana wa Dodawa, kutoka muji wa Maresa, akatoa unabii juu ya Yosafati, akisema: “Kwa sababu umejiunga na Ahazia, Yawe atavunja mashua zote mulizotengeneza.” Na mashua zile zilivunjikavunjika; kwa hiyo hazikuweza kusafiri mpaka Tarsisi. Yosafati akakufa na kuzikwa pamoja na babu zake katika makaburi ya kifalme katika muji wa Daudi; naye Yoramu mwana wake akatawala pahali pake. Yoramu alikuwa na wandugu, wana wa Yosafati; Azaria, Yehieli, Zakaria, Azaria, Mikaeli na Sefatia. Baba yao aliwapa zawadi kubwakubwa za feza, zahabu na vitu vingine vya bei kali, na vilevile miji ya Yuda yenye kuta. Lakini kwa sababu Yoramu ndiye aliyekuwa muzaliwa wake wa kwanza, Yosafati akamupa ufalme atawale kwa pahali pake. Yoramu alipoikalia kiti cha kifalme na utawala wake ulipokuwa umekwisha kuimarika, yeye akawaua wandugu zake wote kwa upanga, na vilevile wakubwa wamoja wa Israeli. Yoramu alianza kutawala akiwa na umri wa miaka makumi tatu na miwili. Alitawala akiwa kule Yerusalema kwa muda wa miaka minane. Alifuata njia mbaya za mufalme Ahabu na za wafalme wengine wa Israeli kama vile jamaa ya Ahabu ilivyofanya kwa sababu muke wake alikuwa binti ya Ahabu. Akatenda maovu mbele za Yawe, lakini Yawe hakutaka kuangamiza ukoo wa Daudi kwa ajili ya agano alilokuwa amefanya na Daudi vilevile kwa sababu alikuwa ameahidi kwamba wazao wake wataendelea kutawala milele. Wakati wa utawala wa Yoramu, Waedomu waliasi utawala wa Yuda, wakaweka mufalme wao wenyewe. Kwa hiyo, Yoramu pamoja na wakubwa wake na magari yake yote akaondoka akawashambulia Waedomu waliokuwa wamemuzunguka yeye pamoja na wakubwa wake na magari. Hivyo Waedomu wakaasi utawala wa Yuda mpaka sasa. Wakati uleule, vilevile wakaaji wa Libuna nao wakaasi utawala wake kwa sababu Yoramu alikuwa amemwacha Yawe, Mungu wa babu zake. Tena alitengeneza pahali pa kuabudia miungu mingine katika milima ya Yuda na kusababisha wakaaji wa Yerusalema kukosa uaminifu na watu wa Yuda kupotoka. Nabii Elia akamupelekea mufalme Yoramu barua hii: “Yawe, Mungu wa Daudi babu yako, anakulaani kwa sababu haukufuata mwenendo wa Yosafati baba yako, au wa Asa mufalme wa Yuda. Lakini umeifuata mienendo ya wafalme wa Israeli na kuwaongoza watu wa Yuda na wa Yerusalema katika kukosa uaminifu kama vile Ahabu, na wafalme wa jamaa yake waliomufuata walivyoongoza Israeli kukosa uaminifu. Vilevile umewaua wandugu zako, wandugu za baba mumoja waliokuwa watu wema zaidi kuliko wewe. Kwa sababu hiyo, Yawe atawaazibu vikali watu wako, wana wako, wake zako na kuharibu mali yako yote. Wewe mwenyewe utapata ugonjwa mukali wa tumbo, ambao utaongezeka siku kwa siku, mpaka matumbotumbo yako yatoke inje.” Kulikuwa Wafilistini na Waarabu wengine waliokuwa wakikaa karibu na Waetiopia. Hawa, Yawe aliwapandisha hasira kusudi wapigane vita na Yoramu. Basi, wakashambulia inchi ya Yuda, wakanyanganya mali yote iliyokuwa katika nyumba yake na kutwaa wana wake wote na wake zake, isipokuwa Ahazia, mwana wake mudogo. Nyuma ya hayo yote, Yawe akamuletea mufalme ugonjwa wa tumbo usioweza kupona. Aliendelea kugonjwa, na ugonjwa wake ukakuwa unaongezeka siku kwa siku, hata kufikia mwisho wa mwaka wa pili, akakufa katika maumivu makali. Watu hawakuwasha moto kwa kuomboleza kifo chake kama vile walivyowafanyia babu zake. Yoramu alianza kutawala akiwa na umri wa miaka makumi tatu na miwili; akatawala kule Yerusalema kwa muda wa miaka minane. Wakati alipokufa, hakuna mutu yeyote aliyemusikitikia. Alizikwa katika muji wa Daudi, lakini si katika makaburi ya wafalme. Wakaaji wa Yerusalema wakamupa Ahazia mwana mudogo wa Yoramu ufalme, atawale pahali pa baba yake kwa sababu wakubwa wake wote waliuawa na kikundi fulani kilichokuja katika kambi pamoja na Waarabu. Hivyo, Ahazia mwana wa Yoramu, mufalme wa Yuda, akatawala. Ahazia, alianza kutawala akiwa mwenye umri wa miaka makumi ine na miwili, akatawala kutoka Yerusalema kwa muda wa mwaka mumoja. Mama yake aliitwa Atalia, mujukuu wa Omuri. Kwa sababu mama yake alikuwa mushauri wake katika kutenda maovu, naye vilevile alifuata mienendo ya jamaa ya Ahabu. Alitenda maovu mbele ya Yawe kama vile jamaa ya Ahabu ilivyofanya maana hao ndio waliokuwa washauri wake nyuma ya kifo cha baba yake, mpaka kwa kuangamia kwake. Hata akafuata shauri lao, akaenda pamoja na mufalme Yoramu mwana wa Ahabu mufalme wa Israeli kupigana vita na Hazaeli mufalme wa Suria kule Ramoti-Gileadi. Nao Wasuria wakamwumiza Yoramu. Kisha akarudi Yezereheli kusudi apate kutunzwa vidonda alivyopata kule Rama, wakati alipopigana na Hazaeli mufalme wa Suria. Naye Ahazia mwana wa Yoramu mufalme wa Yuda akamutembelea Yoramu mwana wa Ahabu kule Yezereheli kwa sababu alikuwa mugonjwa. Lakini ilikuwa imepangwa na Mungu kwamba maangamizi yatendeke kwa Ahazia kwa njia hiyo ya kumutembelea Yoramu; kwa sababu alipofika kule, alitoka pamoja na Yoramu kwenda kupigana na Yehu mwana wa Nimusi ambaye Yawe alimuchagua kwa kuangamiza uzao wa Ahabu. Wakati Yehu alipokuwa akiwahukumu watu wa jamaa ya Ahabu alikutana na wakubwa wa Yuda pamoja na wana wa wandugu za Ahazia, waliomutumikia Ahazia, akawaua. Akamutafuta Ahazia, naye akakamatwa akiwa amejificha kule Samaria. Wakamuleta mpaka kwa Yehu, akauawa. Wakauzika mwili wake maana walisema: “Yeye ni mujukuu wa Yosafati, ambaye alimutafuta Yawe kwa moyo wake wote.” Hapakubaki hata mutu mumoja wa jamaa ya Ahazia ambaye angeweza kushika ufalme. Lakini wakati Atalia mama ya Ahazia alipoona kwamba mwana wake ameuawa, alitoka akaangamiza jamii yote ya kifalme ya Yuda. Lakini Yoseba, binti ya mufalme Yoramu alimutwaa Yoasi, akamuchukua kwa siri kutoka kati ya wana wa mufalme waliokuwa karibu kuuawa. Akamuficha yeye pamoja na yaya wake, katika chumba cha kulala. Hivyo Yoseba, binti ya mufalme Yoramu, muke wa kuhani Yoyada, kwa sababu alikuwa dada ya Ahazia, akamuficha Yoasi kusudi Atalia asimwone na kumwua. Naye akakaa nao kwa muda wa miaka sita akiwa amefichwa ndani ya nyumba ya Mungu wakati Atalia alipokuwa akitawala inchi. Katika mwaka wa saba kuhani Yoyada akajipa moyo akafanya mapatano na majemadari: Azaria mwana wa Yoramu, Isimaeli mwana wa Yohanani, Azaria mwana wa Obedi, Maseya mwana wa Adaya, na Elisafati mwana wa Zikiri. Wakazunguka katika miji yote ya Yuda wakiwakusanya Walawi na viongozi wa makabila ya Israeli, wakaenda mpaka Yerusalema. Mukutano wote ukafanya agano na mufalme katika nyumba ya Mungu. Yoyada akawaambia: “Muangalie huyu mwana wa mufalme! Mumwache atawale kulingana na ahadi Yawe aliyotoa juu ya uzao wa Daudi. Hivi ndivyo mutakavyofanya: sehemu moja ya tatu ya kundi lenu ninyi makuhani na Walawi mutakaoshika zamu siku ya Sabato, mutalinda milango, sehemu moja ya tatu ingine italinda nyumba ya kifalme na sehemu iliyobakia mutalinda Mulango wa Musingi. Watu wote watakuwa katika viwanja vya nyumba ya Yawe. Asikubaliwe mutu mwingine yeyote kuingia ndani ya nyumba ya Yawe isipokuwa makuhani tu pekee na wale Walawi watakaokuwa wanatumika. Hao wanaweza kuingia kwa sababu wao ni watakatifu, lakini wale watu wengine wote, watatii amri ya Yawe. Walawi watamuzunguka mufalme, kila mutu na silaha yake katika mukono; na mutu yeyote atakayejaribu kuingia katika nyumba ya Yawe, atauawa. Mukae na mufalme anapoingia ndani na anapotoka inje.” Walawi na watu wa Yuda walitii amri zote kuhani Yoyada alizotoa. Kila mukubwa akawatwaa watu wake wote, wale waliokuwa wamemaliza zamu na wale waliokuwa wanaingia kushika zamu siku ya Sabato; kwa sababu Yoyada hakuwaruhusu waondoke. Kisha kuhani Yoyada akawapa majemadari mikuki na ngao kubwa na ndogo zilizokuwa mali ya mufalme Daudi, na ambazo zilikuwa zimewekwa katika nyumba ya Yawe. Kisha, akawapanga watu wote kuanzia upande wa kusini mpaka upande wa kaskazini wa nyumba na kuzunguka mazabahu na nyumba, kila mumoja silaha yake katika mikono, kwa kumulinda mufalme. Halafu wakamutoa mwana wa mufalme inje wakamuvalisha taji juu ya kichwa, na kumupa ule ushuhuda; wakamuweka kuwa mufalme nao Yoyada na wana wake wakamupakaa mafuta kisha watu wakashangilia wakisema: “Mufalme aishi milele!” Naye Malkia Atalia aliposikia sauti za watu wakikimbia na kumushangilia mufalme akawaendea hao watu waliokuwa katika nyumba ya Yawe. Alipochungulia akamwona mufalme mupya akisimama karibu na nguzo kwenye mulango, wakati majemadari na wapiga baragumu wakiwa kando ya mufalme na wakaaji wote wakishangilia na kupiga baragumu; nao waimbaji wakiwa na ala zao za muziki wakiongoza watu katika sherehe; halafu akapasua nguo yake na kusema kwa sauti kubwa: “Uasi! Uasi!” Kisha kuhani Yoyada akawatoa inje majemadari wa jeshi akisema: “Mumutoe Atalia inje katikati ya waaskari; yeyote atakayemufuata auawe kwa upanga,” kwa sababu hakutaka wamwue katika nyumba ya Yawe. Basi, wakamukamata, na akaingia katika njia ya mulango wa Farasi wa nyumba ya kifalme, wakamwua huko. Yoyada akafanya agano kati yake mwenyewe, watu wote, na mufalme kwamba watakuwa watu wa Yawe. Halafu watu wote wakaenda kwenye nyumba ya Bali na kuibomoa wakavunja mazabahu pamoja na sanamu zake, hata wakamwua Matani, kuhani wa Bali, mbele ya mazabahu. Kuhani Yoyada akaweka walinzi kwa kulinda nyumba ya Yawe. Hao walinzi wakasimamiwa na makuhani na Walawi ambao Daudi aliwaweka katika kazi ya kutunza nyumba ya Yawe kutoa sadaka za kutetezwa kwa moto kwa Yawe kama vile ilivyoandikwa katika Sheria ya Musa, wakishangilia na kuimba kwa kufuata amri ya Daudi. Vilevile wakasimamia mambo ya uimbaji na sherehe. Akaweka walinzi kwenye milango ya nyumba ya Yawe kusudi mutu yeyote anayehesabiwa kuwa muchafu kwa njia moja au nyingine asiingie. Alitwaa majemadari wa jeshi, waheshimiwa, watawala wa watu, na wakaaji wote; nao wakamusindikiza mufalme kutoka nyumba ya Yawe, wakapitia katika mulango wa juu mpaka kwenye nyumba ya kifalme. Kisha wakamuikalisha mufalme kwenye kiti cha kifalme. Kwa hiyo wakaaji wote wakajaa na furaha; na muji wote ukakuwa mutulivu nyuma ya Atalia kuuawa kwa upanga. Yoasi alikuwa na umri wa miaka saba alipoanza kutawala. Alitawala kwa muda wa miaka makumi ine kule Yerusalema. Mama yake alikuwa Sibia kutoka Beri-Seba. Wakati wote kuhani Yoyada alipokuwa muzima, Yoasi alitenda mema mbele ya Yawe. Yoyada akamwoea wake wawili, nao wakamuzalia wana na wabinti. Nyuma ya hayo Yoasi akaamua kujenga nyumba ya Yawe. Basi, akawaita makuhani na Walawi na kuwaamuru: “Mwende katika miji ya Yuda, mukusanye feza kutoka kwa Waisraeli wote kwa kujenga upya nyumba ya Mungu wenu kila mwaka. Mufanye haraka.” Lakini Walawi hawakufanya haraka. Basi mufalme akamwita kiongozi Yoyada, akamwuliza: “Mbona haujaamurisha Walawi kukusanya kutoka kwa watu wa Yuda na Yerusalema, kodi ambayo Musa mutumishi wa Yawe aliagiza watu walipe kwa ajili ya Hema Takatifu la Yawe?” Kwa sababu wana wa Atalia, yule mwanamuke mwovu walivunja nyumba ya Mungu na kuingia ndani; vilevile vyombo vitakatifu vya nyumba ya Yawe walivitumia katika ibada za Mabali. Basi mufalme akawaamuru, watengeneze sanduku la matoleo na kuliweka inje ya mulango wa nyumba ya Yawe. Kisha tangazo likatolewa kote katika Yuda na Yerusalema, kwamba watu wote wamuletee Yawe kodi ambayo Musa mutumishi wa Mungu, aliwaamuru Waisraeli walipokuwa katika jangwa. Wakubwa wote na watu wote wakafurahi wakaleta kodi yao wakaitumbukiza kwenye sanduku mpaka walipomaliza kufanya hivyo. Walawi walipopeleka sanduku hilo kwa wakubwa wa mufalme, nao walipoona kwamba kuna kiasi kikubwa cha feza ndani, katibu wa mufalme pamoja na musimamizi wa Kuhani Mukubwa, wakazitoa ndani ya sanduku, kisha wakalirudisha kwa nafasi yake. Waliendelea kufanya vile kila siku, wakakusanya feza nyingi. Mufalme na Yoyada walitoa feza zile na kuwapa wale waliosimamia kazi ya kujenga upya nyumba ya Yawe. Nao wakalipa wajengaji, waseremala kwa kutengeneza nyumba ya Yawe. Wakalipa vilevile wafuaji wa chuma na shaba kwa kujenga upya nyumba ya Yawe. Hivyo wafundi hao walishugulika na kazi hiyo kwa bidii, wakairudisha nyumba ya Yawe katika hali yake ya zamani, na kuiimarisha. Walipomaliza kutengeneza nyumba ya Yawe, wakamuletea mufalme na Yoyada zahabu na feza iliyobaki; halafu vyombo kwa ajili ya nyumba ya Yawe vilitengenezwa kwa feza hizo, vyombo hivyo vilikuwa vya kutumika katika kazi ya nyumba ya Yawe, matoleo ya sadaka za kuteketeza kwa moto na mabakuli ya kufukizia ubani, vilevile vyombo vya zahabu na vya feza. Watu waliendelea kutoa sadaka za kuteketezwa kwa moto katika nyumba ya Yawe wakati wote wa Yoyada. Lakini Yoyada akazeeka na alipofikisha umri wa miaka mia moja na makumi tatu, akakufa. Wakamuzika katika muji wa Daudi, kwenye makaburi ya wafalme kwa kuonyesha heshima yao kwake kwa sababu alifanya mema katika Israeli na mbele ya Mungu na nyumba yake. Nyuma ya kifo cha Yoyada, wakubwa wa Yuda wakamwendea mufalme Yoasi wakainama uso mpaka chini mbele yake, wakamushawishi, naye akakubaliana nao. Basi, watu wakaacha kuabudu katika nyumba ya Yawe, Mungu wa babu zao, wakaanza kuabudu Maashera na sanamu. Kasirani ya Mungu ikawaka juu ya Yuda na Yerusalema kwa sababu ya kosa lile. Hata hivyo, akawatumia manabii kwa kuwaonya kusudi wamurudilie Yawe, lakini wao hawakuwasikiliza. Halafu Roho wa Mungu akamujaza Zakaria mwana wa kuhani Yoyada, naye akasimama mbele ya watu kwa pahali palipokuwa juu kidogo, akawaambia: “Yawe anauliza: Kwa nini mumevunja sheria zake? Sasa hamuwezi kufanikiwa! Kwa vile mumemwacha, naye vilevile amewaacha!” Lakini wakamufanyia shauri baya; na kwa amri ya mufalme, wakamupiga mawe kwenye kiwanja cha nyumba ya Yawe. Mufalme Yoasi akasahau mema yote aliyotendewa na Yoyada, baba ya Zakaria, akamwua mwana wake. Alipokuwa karibu kufa, alisema: “Yawe uangalie mambo haya na kuyalipiza.” Kwa mwisho wa mwaka, jeshi la Wasuria lilishambulia Yerusalema na Yuda. Wakawaua wakubwa wote, wakanyanganya vitu vingi na kuvituma kwa mufalme wa Damasiki. Ingawa jeshi la Suria lilikuwa dogo, Yawe alilipatia ushindi mbele ya jeshi kubwa la watu wa Yuda kwa sababu hao watu wa Yuda walikuwa wamemwacha Yawe, Mungu wa babu zao. Hivi, Wasuria wakatimiza azabu ya Mungu juu ya mufalme Yoasi. Waadui walipoondoka, wakamwacha akiwa ameumizwa vibaya sana, wakubwa wake wakamufanyia shauri baya, wakamwua juu ya kitanda chake, kwa kulipiza kisasi cha mauaji ya mwana wa kuhani Yoyada. Alizikwa katika muji wa Daudi, lakini si kwenye makaburi ya wafalme. Watu waliomufanyia shauri baya walikuwa ni Zabadi mwana wa mwanamuke Mwamoni jina lake Simeati, na Yozabadi mwana wa mwanamuke Mumoabu jina lake Simuriti. Habari za wana wake, za kujenga upya nyumba ya Yawe, na unabii wote juu yake, zimeandikwa katika maelezo ya kitabu cha Wafalme. Amazia mwana wake akatawala pahali pake. Amazia alikuwa na umri wa miaka makumi mbili na mitano alipoanza kutawala, akatawala kwa muda wa miaka makumi mbili na mitano katika Yerusalema. Mama yake aliitwa Yoadani wa Yerusalema. Alitenda kwa usawa mbele ya Yawe ingawa hakutenda kwa moyo mukamilifu. Mara tu Amazia alipojiimarisha katika mamlaka akawaua watumishi waliomwua mufalme baba yake. Lakini hakuwaua watoto wao, kama vile ilivyoandikwa katika sheria zinazokuwa katika kitabu cha Musa, ambamo Yawe anatoa amri akisema: “Wazazi hawatauawa kwa ajili ya watoto wao, wala watoto hawatauawa kwa ajili ya wazazi wao; lakini kila mutu atauawa kwa ajili ya zambi zake mwenyewe.” Mufalme Amazia akawakusanya wanaume wa Yuda, akawapanga katika vikundi mbalimbali kulingana na ukoo zao, akawaweka chini ya majemadari wa maelfu na wa mamia kwa ajili ya Yuda na Benjamina. Alipowakagua wale wenye miaka makumi mbili na zaidi, akapata watu elfu mia tatu kwa jumla. Wote walikuwa watu waliochaguliwa wanaofaa kwa vita, wanaoweza kutumia mikuki na ngao. Tena, alilipa waaskari wengine mashujaa elfu moja kutoka Israeli, kwa bei ya kilo elfu tatu za feza. Lakini mutu wa Mungu akamwendea na kumwambia: “Ee mufalme, usiende kwenye vita pamoja na hawa waaskari wa Israeli, maana Yawe hayuko pamoja na watu wa Israeli. Hayuko pamoja na hawa Waefuraimu wote. Lakini ukitaka kwenda, basi ufanye vile, ukuwe hodari katika vita, lakini Mungu atakufanya ushindwe na waadui, kwa maana Mungu ana nguvu kwa kusaidia au kumufanya mutu ashindwe.” Amazia akamwuliza yule mutu wa Mungu: “Tutafanya nini na feza yote ambayo nimekwisha wapa waaskari wa Israeli?” Naye akamujibu: “Yawe anaweza kukupa zaidi ya hiyo.” Kwa hiyo Amazia akawaacha waaskari waliotoka Efuraimu warudi kwao. Basi wakarudi kwao wakiwa wamewakasirikia sana watu wa Yuda. Amazia akajipa moyo akaongoza jeshi lake mpaka kwenye Bonde la Chumvi. Hapo akapigana na kuwaua watu elfu kumi wa Seiri. Na wengine watu elfu kumi, wakakamatwa na kuwapandisha juu ya jiwe kubwa na kuwatupa chini toka juu ya jiwe, wakavunjika vipandevipande. Wakati uleule, wale waaskari Waisraeli ambao Amazia aliwaacha warudi kwao akiwakataza wasijiunge naye katika vita, wakakwenda na kuishambulia miji ya Yuda, toka Samaria mpaka Beti-Horoni, wakaua watu elfu tatu na kunyanganya vitu vingi. Amazia aliporudi kisha kuwashinda Waedomu, akaleta miungu ya Waedomu akaifanya kuwa miungu yake, akainama uso mpaka chini mbele yao na kuifukizia ubani. Hayo yakamukasirisha sana Yawe, akatuma nabii kwa Amazia. Nabii huyo akamwuliza Amazia: “Kwa nini unategemea miungu ya watu wengine ambayo hata haikuweza kuwaokoa watu wake wenyewe kutoka katika mikono yako?” Na alipokuwa angali akisema naye, Amazia akamwambia: “Nyamaza! Tulikufanya wewe kuwa mushauri wa mufalme? Kwa nini uawe?” Nabii akanyamaza, lakini akasema: “Ninafahamu kwamba Mungu ameamua kukuangamiza kwa maana umetenda haya yote, kisha unazarau shauri langu.” Basi Amazia mufalme wa Yuda alifanya shauri, akatuma ujumbe kwa Yoasi, mwana wa Yoahazi, mwana wa Yehu mufalme wa Israeli, akamwambia: “Kuja tuonane uso kwa uso.” Lakini Yoasi mufalme wa Israeli akamupelekea Amazia ujumbe akisema: “Siku moja, muti wa mubaruti wa Lebanoni ukauambia mwerezi nao ni wa kule hivi: ‘Umwoeshe binti yako kwa mwana wangu!’ Lakini nyama mumoja wa pori akapita pale na kukanyagakanyaga mubaruti ule. Sasa wewe Amazia unasema: ‘Nimewaua Waedomu’ na moyo unakufanya ujivune. Basi, ikaa ndani ya nyumba yako; kwa nini kujitafutia taabu zitakazokuangamiza wewe mwenyewe pamoja na watu wako wa Yuda?” Lakini Amazia hakujali kwa maana lilikuwa kusudi la Mungu apate kuwekwa katika mukono wa waadui zao kwa sababu alitegemea miungu ya Edomu. Kwa hiyo, Yoasi, mufalme wa Israeli akatoka akapambana uso kwa uso na Amazia, mufalme wa Yuda katika vita kule Beti-Semesi, katika inchi ya Yuda. Watu wa Yuda wakashindwa na watu wa Israeli na kila mumoja akarudia kwake. Halafu Yoasi mufalme wa Israeli alimukamata Amazia mufalme wa Yuda, mwana wa Yoasi, mwana wa Ahazia kule Beti-Semesi akamupeleka mpaka Yerusalema. Kule, akabomoa ukuta wa muji ule, kuanzia kwenye mulango wa Efuraimu mpaka kwenye mulango wa Pembeni, umbali wa karibu metre mia mbili. Akatwaa zahabu yote na feza hata na vifaa vyote vilivyokuwa katika nyumba ya Yawe chini ya ulinzi wa Obedi-Edomu; vilevile akatwaa hazina ya nyumba ya kifalme mateka, kisha akarudi Samaria. Amazia mufalme wa Yuda aliishi miaka kumi na mitano nyuma ya kifo cha mufalme Yoasi mwana wa Yoahazi mufalme wa Israeli. Matendo mengine yote ya Amazia kutoka mwanzo mpaka mwisho yameandikwa katika Kitabu cha Wafalme wa Yuda na Israeli. Mashauri mabaya ya kumwua Amazia yalifanywa Yerusalema tangu alipomwacha Yawe, kwa hiyo akakimbilia Lakisi. Lakini waadui wakatuma watu Lakisi wakamwua kule. Maiti yake ikaletwa juu ya farasi, na kuzikwa kwenye makaburi ya kifalme katika muji wa Daudi. Kisha watu wote wa Yuda wakamukamata Uzia mwana wa Amazia akiwa mwenye umri wa miaka kumi na sita, wakamufanya kuwa mufalme pahali pa Amazia baba yake. Halafu nyuma ya kifo cha baba yake akajenga upya muji wa Eloti na kuurudisha kwa inchi ya Yuda. Uzia alianza kutawala akiwa na umri wa miaka kumi na sita; akatawala kwa muda wa miaka makumi tano na miwili kule Yerusalema. Mama yake aliitwa Yekolia wa Yerusalema. Alitenda kwa usawa mbele ya Yawe, kama vile baba yake alivyotenda. Akamutumikia Yawe kwa uaminifu wakati wa kuishi kwa Zakaria, aliyemufundisha kumutii Mungu. Kwa jinsi alivyomutafuta Mungu, Mungu alimufanikisha. Uzia akaondoka kwa kupigana vita na Wafilistini, akabomoa kuta za miji ya Gati, Yabune na Asidodi. Akajenga miji katika eneo la Asidodi na fasi ingine katika inchi ya Filistia. Mungu akamusaidia kuwashinda Wafilistini, Waarabu waliokaa Guribali na Wameuni. Waamoni walimulipa kodi, na sifa zake zikaenea mpaka Misri, kwa sababu alipata nguvu. Tena Uzia akajenga minara ya kukinga muji kwenye milango tatu ya Yerusalema na kuiimarisha. Hata katika jangwa vilevile alijenga minara, akachimba visima vingi, maana alikuwa na makundi mengi ya nyama kwenye sehemu za miinuko na mabonde. Alikuwa na walimaji na watunza mizabibu kwenye milima, na katika inchi yenye mboleo maana alipenda mulimo. Zaidi ya hayo, Uzia alikuwa na jeshi lililokuwa tayari kwa vita. Lilikuwa limegawanywa katika vikundi mbalimbali, na jumla ya hesabu yao iliwekwa na katibu Yeieli, na Masea, mukubwa, nao wote walikuwa chini ya uongozi wa Hanania, mumoja wa majemadari wa mufalme. Kwa jumla, viongozi wote wa majeshi walikuwa elfu mbili na mia sita. Chini yao, kulikuwa jeshi la waaskari elfu mia tatu na saba na mia tano, wenye uwezo mukubwa wa kupigana na waadui wa mufalme. Uzia aliwapa waaskari wale ngao, mikuki, kofia za chuma, nguo za chuma, pinde na mawe kwa ajili ya kupiga mujeledi. Kule Yerusalema wafundi wake wakamutengenezea mitambo ya kurushia mishale na mawe makubwamakubwa. Sifa zake zikaenea kila pahali, nguvu zake zikaongezeka zaidi kwa sababu ya usaidizi mwingi alioupata kutoka kwa Mungu. Lakini wakati mufalme Uzia alipokuwa na nguvu, moyo wake akajaa kiburi ambacho kilisababisha maangamizi yake. Akamwasi Yawe wake kwa kuingia ndani ya hekalu akikusudia kufukiza ubani juu ya mazabahu. Lakini kuhani Azaria, pamoja na makuhani wengine mashujaa makumi nane, wakamufuata mufalme na kumuzuia. Wakamwambia: “Si kazi yako hata kidogo Uzia, kumufukizia Yawe ubani. Ni makuhani tu wa uzao wa Haruni ambao wametakaswa kwa kufukiza ubani. Ondoka pahali hapa patakatifu. Umemukosea Yawe na hautapata heshima yoyote kutoka kwake.” Wakati ule, Uzia alikuwa amesimama ndani ya hekalu karibu na mazabahu, akishika chetezo cha kufukizia ubani katika mukono. Akawakasirikia makuhani; na mara tu alipofanya hivyo, akashikwa na ukoma katika paji la uso wake mbele ya makuhani hao. Azaria, Kuhani Mukubwa, na wale makuhani wengine, wakamwangalia, kisha wakaharakisha kumutoa inje; hata yeye mwenyewe akafanya haraka kutoka, kwa maana Yawe alikuwa amemwazibu. Basi mufalme Uzia akakuwa na ukoma mpaka siku ya kufa kwake. Alikaa katika nyumba yake ya pekee maana hakukubaliwa tena kuingia katika nyumba ya Yawe. Na Yotamu mutoto wake, akatunza jamaa yake akitawala wakaaji wa inchi. Matendo mengine yote ya mufalme Uzia kutoka mwanzo mpaka mwisho, yaliandikwa na nabii Isaya mwana wa Amozi. Uzia akakufa na kuzikwa katika eneo la kuzikia wafalme, kwa sababu walisema: “Yeye ana ukoma”. Naye Yotamu mwana wake, akatawala pahali pake. Yotamu alikuwa na umri wa miaka makumi mbili na mitano alipoanza kutawala, alitawala kwa muda wa miaka kumi na sita kule Yerusalema. Mama yake aliitwa Yerusa binti ya Sadoki. Alitenda kwa usawa mbele ya Yawe kama vile Uzia baba yake alivyotenda. Hakuingia katika hekalu la Yawe. Watu waliendelea kufanya maovu. Yotamu alijenga mulango wa kaskazini wa nyumba ya Yawe na kushugulika sana na ujenzi wa ukuta sehemu ya Ofeli. Alijenga miji kwenye inchi ya milima ya Yuda, na kwenye pori, akajenga makimbilio na minara katika milima yenye pori. Alipigana vita na mufalme wa Amoni na kuwashinda. Katika mwaka ule Waamoni wakamutolea kodi ya kilo elfu tatu na mia ine za feza, toni elfu moja za ngano na kilo elfu moja za shayiri, waliendelea kufanya hivyo katika mwaka wa pili na wa tatu. Mufalme Yotamu aliendelea kuwa mwenye nguvu, kwa sababu aliishi kwa kumutii Yawe, Mungu wake. Matendo mengine ya Yotamu, vita yake na maongozi yake, yote yameandikwa katika Kitabu cha Wafalme wa Israeli na Yuda. Yotamu alikuwa na umri wa miaka makumi mbili na mitano alipoanza kutawala, akatawala kwa muda wa miaka kumi na sita kule Yerusalema. Akakufa na kuzikwa katika muji wa Daudi. Na Ahazi mwana wake akatawala pahali pake. Ahazi alianza kutawala akiwa na umri wa miaka makumi mbili, alitawala kwa muda wa miaka kumi na sita kule Yerusalema. Yeye, hakufuata mufano muzuri wa Daudi babu yake, lakini alitenda maovu mbele za Yawe, na kufuata mienendo ya wafalme wa Israeli. Vilevile, alitengeneza hata sanamu za Mabali za madini yenye kuyeyushwa, akafukiza ubani kwenye Bonde la mwana wa Hinomu na kuwateketeza wana wake kama sadaka, akiiga desturi za kuchukiza za watu ambao walifukuzwa na Yawe wakati Waisraeli walipokuwa wanaingia katika inchi. Alitoa sadaka na kufukiza ubani pahali pa kuabudia miungu mingine, juu ya vilima na chini ya kila muti wenye majani mabichi. Yawe, Mungu wake akamwacha mufalme Ahazi ashindwe na mufalme wa Suria ambaye vilevile akawapeleka watu wake wengi, akarudi nao Damasiki. Vilevile, alimufanya ashindwe na mufalme wa Israeli ambaye alimushinda na kuua watu wengi sana. Peka, mwana wa Remalia akawaua watu wengi sana. Aliua waaskari mashujaa wa Yuda elfu mia moja na makumi mbili katika siku moja. Ilitokea vile kwa sababu walimwacha Yawe, Mungu wa babu zao. Zikiri, askari mumoja shujaa wa Israeli, alimwua Maseya, mwana wa mufalme, Azirikamu, musimamizi wa nyumba ya kifalme, na Elekana aliyekuwa mutu wa pili kwa mufalme. Jeshi la Israeli likapeleka wafungwa wandugu zao watu elfu mia mbili, wanawake na watoto. Waliwapeleka mpaka Samaria pamoja na mali nyingi waliyonyanganya. Lakini kule Samaria kulikuwa nabii wa Yawe, jina lake Obedi. Yeye alitoka kwenda kukutana na waaskari wa Israeli walipokuwa karibu kuingia Samaria, akawaambia: “Yawe, Mungu wa babu zenu, alikuwa amewakasirikia watu wa Yuda, ndiyo maana aliwatia katika mikono yako lakini umewaua kwa hasira. Tendo hilo limetoka mbinguni. Sasa munakusudia kuwafanya wanaume na wanawake wa Yuda na Yerusalema watumwa wenu. Hamutambui kwamba ninyi vilevile mumetenda zambi mbele ya Yawe, Mungu wenu? Sasa sikia yale ninayosema, muwarudishe wandugu zenu na wadada zenu muliowakamata kuwa wafungwa, maana kasirani kali ya Yawe iko juu yenu.” Nao wakubwa fulani wa Efuraimu, Azaria mwana wa Yohana, Berekia mwana wa Mesilemoti, Yehizikia mwana wa Salumu na Amasa mwana wa Hadilai, vilevile waliwagombeza wale waliotoka kwa vita. Wakawaambia: “Musiwalete humu wafungwa hao, kwa sababu munakusudia kutuletea kosa mbele ya Yawe, tendo hili huku litakuwa nyongezo ya zambi yetu na kosa letu; kwa sababu kosa letu tayari ni kubwa na kuna kasirani kali juu ya Israeli.” Hivyo, waaskari wakawaacha wafungwa wao na vitu vyote walivyonyanganya katika mikono ya wakubwa na mukutano wote. Wale wakubwa waliotajwa majina yao waliwatwaa wafungwa na kwa kutumia vitu vilivyonyanganywa wakawavalisha wafungwa ambao hawakukuwa na nguo; waliwapatia viatu, chakula na vinywaji, na kuwapakaa mafuta. Wale ambao walikuwa hawajiwezi, wakawabeba juu ya punda, wakawapeleka wafungwa wote mpaka Yeriko, muji wa mingazi, kwa wandugu zao; kisha wao wakarudi Samaria. Wakati ule, mufalme Ahazi akatuma wajumbe kwa mufalme wa Asuria kusudi awasaidie kwa sababu Waedomu walikuwa wamekuja tena, wakashambulia inchi ya Yuda, wakawashinda na kupeleka wafungwa wengi. Wakati uleule, Wafilistini walikuwa wakiishambulia miji ya Sefela na Negebu ya Yuda. Walinyanganya miji ya Beti-Semesi, Ayaloni, Gederoti, Soko na vijiji vyake, Timuna na vijiji vyake, Gimuzo na vijiji vyake, wakafanya makao yao kule. Kwa maana Yawe alinyenyekeza inchi ya Yuda kwa ajili ya Ahazia mufalme wa Israeli sababu yeye alifanya uasherati katika Yuda na kumwasi Yawe. Tigilati-Pileseri, mufalme wa Asuria akamushambulia pahali pa kumutia nguvu. Kwa sababu Ahazi alitwaa zahabu kutoka katika nyumba ya Mungu, nyumba ya kifalme na nyumba za wakubwa, akamupa mufalme wa Asuria kama kodi; lakini jambo hili vilevile halikumusaidia kwa kitu. Wakati alipokuwa katika taabu zaidi, mufalme huyu Ahazi alizidi kumwasi Yawe. Kwa sababu alitolea sadaka kwa miungu ya Damasiki iliyokuwa imemushinda katika vita akisema: “Kwa sababu miungu ya Suria iliwasaidia wafalme wa Shamu, nikiitolea sadaka labda itanisaidia nami vilevile.” Lakini ilisababisha kuangamia kwake na taifa lote la Israeli. Zaidi ya hayo, alikusanya vifaa vyote vya nyumba ya Mungu, akavikatakata vipandevipande, kisha akafunga milango ya nyumba ya Yawe na kujijengea mazabahu katika kila pembe ya Yerusalema. Na katika kila muji wa Yuda, akatengeneza pahali pa kufukizia ubani kwa miungu mingine. Kwa kutenda hivyo, akamukasirikisha Yawe, Mungu wa babu zake. Matendo yake mengine na mienendo yake yote, kutoka mwanzo mpaka mwisho, yameandikwa katika Kitabu cha Wafalme wa Yuda na Israeli. Mufalme Ahazi alikufa na kuzikwa katika muji wa Yerusalema, lakini si katika makaburi ya wafalme wa Israeli. Na Hezekia mwana wake, akatawala pahali pake. Hezekia alianza kutawala Yuda akiwa na umri wa miaka makumi mbili na mitano, akatawala kule Yerusalema kwa muda wa miaka makumi mbili na tisa. Mama yake aliitwa Abiya binti ya Zakaria. Alitenda kwa usawa mbele ya Yawe, kama vile babu yake Daudi alivyotenda. Katika mwezi wa kwanza wa mwaka wa kwanza wa utawala wake, mufalme Hezekia akafungua tena milango ya hekalu, akaitengeneza. Akawaingiza makuhani na Walawi, kisha akawakusanya katika kiwanja upande wa mashariki, akawaambia: “Munisikilize, enyi Walawi! Mujitakase na mutakase nyumba ya Yawe, Mungu wa babu zenu. Mutoshe uchafu wote unaokuwa katika Pahali Patakatifu. Kwa maana babu zetu waliasi na kutenda maovu mbele ya Yawe, Mungu wetu. Wamemwacha na kugeuzia mbali nyuso zao na makao ya Yawe. Tena, wamefunga milango ya baraza, wakazimisha taa, na hawajafukiza ubani wala kutoa sadaka za kuteketeza kwa moto katika Pahali Patakatifu pa Mungu wa Israeli. Kwa sababu hii, Yawe akakasirikia sana inchi ya Yuda na Yerusalema, na yale aliyowatendea yalikuwa ya kushangaza, ya kuogopesha na ya kuchekelewa. Haya yote mumeyaona wenyewe kwa macho yenu. Baba zetu waliuawa katika vita, na wana wetu na wabinti zetu na wake zetu ni wafungwa kwa sababu hii. Sasa, nimeamua ndani ya moyo wangu kufanya agano na Yawe, Mungu wa Israeli, kusudi asitukasirikie zaidi. Basi wana wangu, musikuwe wavivu. Yawe amewachagua ninyi kusudi mumutumikie, muwaongoze watu wake katika ibada, na kumufukizia ubani.” Hawa wakawakusanya Walawi wenzao, wakajitakasa. Kisha wakaingia kama walivyotakiwa kufanya na mufalme, wakaanza kusafisha nyumba ya Yawe kama vile Yawe alivyoagiza. Makuhani wakaingia katika sehemu ya ndani ya nyumba ya Yawe, wakatosha uchafu wote uliokuwa mule, wakauweka katika kiwanja. Kutoka pale, Walawi walitwaa uchafu ule mpaka inje kwenye Bonde la Kidroni. Walianza kazi ya kutakasa hekalu siku ya kwanza ya mwezi wa kwanza, na kufikia siku ya nane, wakakuwa wamekwisha kumaliza kazi yote, hata na baraza. Kisha, wakafanya kazi kwa muda wa siku nane zaidi mpaka siku ya kumi na sita ya mwezi ule, kila kitu kikakamilika. Kisha, Walawi wakamwendea mufalme Hezekia wakamwambia: “Tumekwisha kutakasa hekalu lote pamoja na mazabahu ya sadaka za kuteketeza kwa moto na vyombo vyake vyote, na meza ya mikate inayotolewa kwa Mungu na vyombo vyake vyote. Tena, tumerudisha na kutakasa vyombo vyote ambavyo mufalme Ahazi alivyotupa wakati wa utawala wake, pale alipoasi. Vyote vipo mbele ya mazabahu ya Yawe.” Bila kupoteza wakati, mufalme Hezekia akawakusanya wakubwa wa muji, akaenda nao katika nyumba ya Yawe. Wakaleta ngombe dume saba, kondoo dume saba, wana-kondoo saba na mbuzi dume saba, kuwa sadaka ya maondoleo ya zambi, kwa ajili ya jamaa ya kifalme, ya Pahali Patakatifu na ya watu wa Yuda. Kwa hiyo, mufalme akawaambia makuhani waliokuwa wazao wa Haruni wawateketeze juu ya mazabahu ya Yawe. Makuhani walichinja ngombe dume kwanza, kisha kondoo dume, halafu wana-kondoo na kila mara walitwaa damu ya nyama wale na kuinyunyiza juu ya mazabahu. Kisha, wakawaleta wale mbuzi dume wa sadaka ya maandoleo ya zambi karibu na mufalme na watu wote waliokuwa mule, nao wakaweka mikono yao juu ya mbuzi dume wale. Basi, wale makuhani wakawachinja, na kunyunyiza damu yao juu ya mazabahu kusudi ikuwe sadaka ya upatanisho kwa Waisraeli wote, kwa maana mufalme Hezekia alikuwa ameagiza sadaka ya kuteketeza kwa moto na sadaka ya maondoleo itolewe kwa ajili ya Waisraeli wote. Mufalme Hezekia alifuata maagizo ambayo Yawe alikuwa amemupa mufalme Daudi kwa njia ya Gadi, nabii wa mufalme na nabii Natani. Hivyo basi, akaweka Walawi katika nyumba ya Yawe, wamoja wao wakiwa na matoazi, wengine vinanda na wengine vinubi. Hiyo ilikuwa amri ya Yawe kwa njia ya manabii wake. Walawi walisimama na vyombo vya muziki vya Daudi, vilevile makuhani walisimama wakiwa na baragumu zao. Basi, Hezekia akaamuru sadaka ya kuteketeza kwa moto itolewe juu ya mazabahu. Mara tu sadaka hiyo ilipoanza kutolewa, watu wakaanza kumusifu Yawe kwa nyimbo zilizofuatana na mulio wa baragumu na vyombo vya muziki vya Daudi, mufalme wa Israeli. Watu wote waliokuwa mule wakashiriki katika ibada. Waimbaji wakaendelea na kuimba, na baragumu zikaendelea kupigwa mpaka wakati shuguli za utoaji wa sadaka hiyo ya kuteketeza kwa moto ilipokamilika. Kisha, mufalme Hezekia pamoja na watu wote waliokuwa pale wakainama, kwa kumwabudu Yawe. Kisha mufalme Hezekia na viongozi wakawaambia Walawi wamusifu Yawe kwa nyimbo ambazo mufalme Daudi na nabii Asafu walizotunga. Basi, watu wote wakamutukuza Mungu kwa furaha, na kuinama uso mpaka chini. Halafu Hezekia akawaambia watu: “Sasa mumekwisha kujitakasa, mukaribie, mulete sadaka na matoleo ya shukrani katika nyumba ya Yawe.” Basi, watu wakaleta sadaka zao na matoleo yao ya shukrani, na za kuteketeza. Sadaka za kuteketeza walizoleta kwa jumla zilikuwa ngombe dume makumi saba, kondoo dume mia moja na wana-kondoo mia mbili. Zote hizo zilikuwa sadaka za kuteketeza kwa ajili ya Yawe. Matoleo matakatifu yalikuwa ngombe dume mia sita na kondoo elfu tatu. Kwa vile ambavyo hesabu ya makuhani ilikuwa ndogo, hawakuweza kuchuna nyama wale wote. Kwa hiyo, wandugu zao Walawi wakawasaidia mpaka walipomaliza kazi hiyo. Wakati ule, makuhani wengine zaidi walikuwa wamekwisha kujitakasa. (Walawi walijiweka katika hali ya usafi zaidi kuliko makuhani.) Mbali na wingi wa sadaka za kuteketeza, kulikuwa vilevile mafuta ya sadaka ya amani, hata kulikuwa sadaka ya kinywaji kwa ajili ya kila sadaka za kuteketeza. Hivyo basi, kazi za ibada zikaanzishwa tena katika hekalu. Mufalme Hezekia na watu wote wakajazwa na furaha tele kwa sababu ya yote Mungu aliyowatendea watu; maana tukio hili lilitokea kwa rafla. Mufalme Hezekia akawatumia ujumbe watu wote wa Israeli na Yuda, na vilevile akawaandikia barua watu wa kabila la Efuraimu na Manase, akiwaalika wote wakuje katika nyumba ya Yawe kule Yerusalema, kusudi wafanye sikukuu ya Pasaka kwa heshima ya Yawe, Mungu wa Israeli. Mufalme, viongozi na watu wote wa muji wa Yerusalema walifanya shauri kwa kufanya sikukuu hiyo ya Pasaka katika mwezi wa pili pahali pa mwezi wa kwanza kama vile ilivyokuwa kawaida, kwa sababu hesabu ya makuhani waliokuwa wamekwisha kujitakasa ilikuwa ndogo, nao watu walikuwa bado hawajakusanyika Yerusalema. Mupango huu ukamupendeza mufalme pamoja na watu wote waliokuwa wamekusanyika. Kwa hiyo wakaamua kutoa tangazo katika inchi yote ya Israeli, kutoka Beri-Seba mpaka Dani, kwamba watu wakuje Yerusalema kwa kufanya sikukuu ya Pasaka ya Yawe, Mungu wa Israeli. Ilikuwa imepita muda murefu mbele ya watu kufanya Pasaka kulingana na sheria zake. Kwa hiyo wajumbe wakapita katika inchi yote ya Israeli na ya Yuda kwa kupeleka barua zile kufuatana na amri ya mufalme na wakubwa wake. Barua hizo zilikuwa na ujumbe huu: “Enyi watu wa Israeli muliobaki nyuma ya mashambulizi ya wafalme wa Asuria. Mumurudilie Yawe, Mungu wa Abrahamu, Isaka na Israeli, kusudi naye apate kuwarudilia. Musikuwe kama babu zenu na wandugu zenu ambao hawakukuwa waaminifu kwa Yawe Mungu wa babu zao, ambaye kama vile munavyoona aliwaazibu vikali. Sasa musikuwe wenye mioyo migumu kama babu zenu lakini mumutii Yawe. Mukuje katika Pahali Patakatifu pake Yerusalema, ambako ametakasa milele, mumwabudu Yawe, Mungu wenu, kusudi asiwakasirikie. Mukimurudilia Yawe, wale ambao walipeleka wandugu zenu na watoto wenu kuwa wafungwa, watawahurumia na kuwaacha warudi katika inchi hii. Kwa maana Yawe, Mungu wenu, ni mwenye huruma na rehema, naye hatawageuzia mugongo ikiwa mutamurudilia.” Basi wajumbe wale wakaenda toka muji mumoja mpaka mwingine katika inchi yote ya Efuraimu na Manase, wakafika hata katika inchi ya Zebuluni. Lakini watu waliwacheka na kuwazarau. Hata hivyo, watu wachache kati ya makabila ya Aseri, Manase na Zebuluni, walijinyenyekeza wakakuja Yerusalema. Nguvu za Mungu zilikuwa zikifanya kazi katika Yuda, zikitia moyo wa kutii amri za mufalme na wakubwa wake kadiri ya maagizo ya Yawe. Watu wengi sana wakakusanyika Yerusalema katika mwezi wa pili, kwa kufanya sikukuu ya Mikate Isiyotiwa Chachu. Wakaanza kazi, wakaondoa mazabahu zote zilizokuwa Yerusalema, na zingine zote zilizotumiwa kwa kufukizia ubani, wakazibeba na kuzitupa katika Bonde la Kidroni. Siku ya kumi na ine ya mwezi ule wakachinja mwana-kondoo wa Pasaka. Makuhani na Walawi wakapata haya, wakajitakasa na kuleta sadaka za kuteketezwa katika nyumba ya Yawe. Wakatwaa nafasi zao katika hekalu kulingana na maagizo yaliyokuwa katika Sheria ya Musa, mutu wa Mungu. Walawi wakawapa makuhani damu ya sadaka, nao wakainyunyiza juu ya mazabahu. Kwa vile ambavyo wengi wa wale waliokusanyika pale hawakukuwa wamejitakasa. Walawi walipaswa kuwachinjia wana-kondoo wa Pasaka na kuwatakasa kwa ajili ya Yawe. Watu wengi kati ya wale waliotoka katika kabila la Efuraimu, Manase, Isakari na Zebuluni, walikuwa wakifanya Pasaka kinyume cha maagizo. Hii ni kwa kuwa mufalme Hezekia aliwaombea akisema: “Yawe, wewe ni mwema. Umusamehe mutu yeyote atakayekuomba kwa moyo wake wote wewe Yawe, Mungu wa babu zake, hata ingawa yule mutu si musafi kulingana na sheria za utakaso.” Yawe akakubali ombi la Hezekia, akawasamehe watu wale. Waisraeli wote waliokuwa wamekusanyika Yerusalema wakafanya sikukuu ya Mikate Isiyotiwa Chachu kwa muda wa siku saba, wakiwa na furaha kubwa. Walawi na makuhani wakamusifu Yawe kila siku, walimwimbia kwa nguvu zao zote. Mufalme Hezekia aliwasifu na kuwatia moyo makuhani kwa sababu waliendesha ibada kwa ujuzi mwingi. Nyuma ya kumaliza siku saba ambamo watu walikula, wakatoa sadaka za amani na kumutukuza Yawe, Mungu wa babu zao, watu waliamua kwa shauri moja kuendelesha sherehe kwa muda wa siku saba zaidi. Basi wakaendelea kusherehekea kwa furaha kubwa kwa muda wa siku saba zaidi. Mufalme Hezekia wa Yuda akawapa watu waliokusanyika jumla ya ngombe dume elfu moja na kondoo elfu saba. Vilevile, wakubwa wakawapa ngombe dume elfu moja na kondoo elfu kumi. Hesabu kubwa ya makuhani wakajitakasa. Kila mutu aliyehuzuria alifurahi sana. Watu wote wa Yuda, makuhani na Walawi, wakaaji wa Yerusalema waliohuzuria, wageni waliotoka inje ya Yerusalema na wale walioishi katika inchi ya Yuda, wote walifurahi sana. Kukakuwa furaha kubwa sana Yerusalema, maana tangu wakati wa mufalme Solomono mwana wa Daudi, mufalme wa Israeli jambo kama hilo lilikuwa halijatokea Yerusalema. Kisha, makuhani na Walawi wakawaombea watu baraka za Yawe, naye katika makao yake matakatifu kule mbinguni akasikia maombi yao na kuyakubali. Nyuma ya sherehe kumalizika, watu wote wa Israeli wakakwenda katika kila muji wa Yuda, wakavunjavunja nguzo za mawe na kukatakata sanamu za Ashera, mungu wa kike, na vilevile wakaharibu mazabahu na pahali pa kuabudia miungu mingine. Wakafanya vile katika inchi yote ya Yuda, Benjamina, Efuraimu na Manase, mpaka walipokwisha kuvimaliza vyote. Kisha Waisraeli wakarudi kwao, kila mutu kwenye urizi wake. Mufalme Hezekia akawapanga tena makuhani na Walawi katika makundi, akamupa kila mumoja wao kazi kufuatana na utumishi wake katika sehemu mbalimbali za hekalu la Yawe. Kazi ile ni pamoja na utoaji wa sadaka za kuteketeza kwa moto na za amani, za shukrani na za kusifu. Kutoka mali yake mwenyewe, mufalme akatoa sehemu kwa ajili ya sadaka za kuteketezwa asubui na magaribi, za siku ya Sabato na wakati wa sherehe za mwandamo wa mwezi na zile sikukuu zingine zilizoamuriwa kulingana na Sheria ya Yawe. Zaidi ya hayo, mufalme akawaambia wakaaji wa Yerusalema watoe sehemu makuhani na Walawi waliyostahili kupewa, kusudi wao wajitolee kikamilifu katika shuguli za sheria za Yawe. Mara tu amri hii ilipotolewa, watu wa Israeli wakatoa kwa wingi, malimbuko ya ngano, divai, mafuta, asali na mazao mengine mbalimbali ya shamba, na vilevile sehemu moja ya kumi ya kila kitu. Watu wa Israeli na Yuda walioishi katika miji ya Yuda, wakaleta vilevile sehemu moja ya kumi ya ngombe na kondoo na ya vitu vitakatifu vilivyotolewa kwa Yawe. Wakaviweka vitu hivyo katika mafungu. Katika mwezi wa tatu wakaanza kuvipanga katika mafungu, wakamaliza katika mwezi wa saba. Mufalme Hezekia na wakubwa wake walipokuja kuangalia mafungu yale, wakamushukuru Yawe na watu wake wa Israeli. Mufalme Hezekia akawauliza makuhani na Walawi juu ya mafungu hayo. Azaria, Kuhani Mukubwa aliyekuwa wa uzao wa Sadoki akamujibu: “Tangu wakati watu walipoanza kuleta matoleo yao katika hekalu, tumekuwa na vyakula vya kutosha na hata tuna akiba kubwa. Yawe amewabariki watu wake, ndiyo maana tumepata vitu hivi vyote.” Kisha mufalme Hezekia akawaamuru watengeneze gala katika nyumba ya Yawe. Wakatengeneza; na mule ndani wakaweka matoleo, sehemu moja za kumi na vyote vilivyotakaswa kwa uaminifu. Wakamuweka Konania, Mulawi, kuwa musimamizi mukubwa muchungaji wa vitu hivyo, na ndugu yake, Simea kuwa musaidizi wake. Nao Yehieli, Azazia, Nahati, Asaeli, Yeremoti, Yozabadi, Elieli. Isimakia, Mahati na Benaya, wakawekwa kuwa wasimamizi chini ya uongozi wa Konania na ndugu yake Simei. Hawa wote walichaguliwa na mufalme Hezekia, na Azaria, kuhani mukubwa wa nyumba ya Mungu. Kore mwana wa Imuna, Mulawi, aliyekuwa mulinzi wa Mulango wa Mashariki wa hekalu, akasimamia matoleo yote ya mapenzi kwa Mungu; na kugawanya matoleo kwa ajili ya Yawe na sadaka zinazokuwa takatifu kabisa. Nao Edeni, Miniamini, Yesua, Semaya, Amaria na Sekania, walimusaidia kufanya kazi hiyo kwa uaminifu katika ile miji mingine makuhani walimoishi. Waliwagawanyia wandugu zao Walawi vyakula, kwa wakubwa kama vile kwa wadogo. Tena, bila kujali ukoo walimoandikishwa, waliwapa sehemu wale watoto wa kiume waliokuwa wametimiza umri wa miaka mitatu na zaidi, na ambao waliingia katika nyumba ya Yawe kila siku kwa kutimiza kazi zao. Kila mumoja wao alipata sehemu yake kulingana na kazi aliyofanya kwa zamu yake. Makuhani waliandikishwa kulingana na jamaa zao, na Walawi waliotimiza miaka makumi mbili na zaidi waliandikishwa kulingana na kazi zao na zamu zao. Waliandikishwa wote pamoja na watoto wao wadogo, wake zao, wana wao na wabinti zao kwa sababu, kwa kujitoa kwa kazi zao, walihitajika kujiweka katika hali ya utakaso kila mara. Vilevile, kati ya wazao wa Haruni, makuhani waliokuwa wanakaa katika mashamba waliyorizi kwa pamoja inje ya miji yao, kulikuwa watu waliochaguliwa kwenye miji hiyo ambao waliwagawanyia sehemu zao za vyakula. Waliwapa sehemu kila mwanaume katika jamaa za makuhani, na kila mumoja aliyekuwa ameandikishwa kati ya Walawi. Hivi ndivyo mufalme Hezekia alivyotenda mambo mema, ya haki na ya uaminifu mbele ya Yawe, Mungu wake, katika inchi yote ya Yuda. Kila kazi aliyoifanya katika utumishi wa nyumba ya Mungu au katika kutii sheria na amri za Mungu kwa kufuata uongozi kutoka kwake, alizifanya kwa moyo wake wote, naye akafanikiwa. Nyuma ya matendo hayo ya uaminifu ya mufalme Hezekia, mufalme Saniharibu wa Asuria akashambulia inchi ya Yuda. Akakuja kupiga makambi kwenye miji yenye kuta akitumaini kwamba ataishinda ikuwe mali yake. Mufalme Hezekia alipoona kwamba mufalme Saniharibu amekuja kwa kusudi la kuishambulia Yerusalema, akaamua, yeye pamoja na wakubwa wake na wakubwa wa majeshi kufunga maji ya chemichemi zilizokuwa inje ya miji; nao wakamuunga mukono, wakamusaidia. Wakawakusanya watu wengi pamoja, wakazifunga chemichemi zote pamoja na kijito kilichopitia kati ya sehemu hiyo wakisema: “Kwa nini kuwaachia wafalme wa Asuria, wakikuja wakute maji tele?” Hezekia akajitia moyo, akajenga upya ukuta wote uliokuwa umebomoka, na juu yake akajenga minara. Upande wa inje, akajenga ukuta mwingine wa pili, na akaiimarisha uwanja wa Milo katika muji wa Daudi. Zaidi ya hayo akatengeneza silaha na ngao kwa wingi. Akaweka watu wote wa muji chini ya uongozi wa majemadari, kisha akawaamuru wakusanyike katika uwanja penye Mulango wa Muji. Hapo akawatia moyo akisema: “Muwe imara na hodari. Musiogope wala musifazaike mbele ya mufalme wa Asuria au majeshi yake maana tunayekuwa naye ni mukubwa kuliko anayekuwa na Saniharibu. Yeye ana nguvu za kibinadamu tu, lakini sisi tuna Yawe, Mungu wetu, kwa kutusaidia na kutupigania vita vyetu.” Maneno haya ya mufalme Hezekia yakawatia moyo sana watu wale. Nyuma ya hayo, Saniharibu mufalme wa Asuria, ambaye alikuwa angali anauzunguka muji wa Lakisi akiwa na majeshi yake yote, akawatuma watumishi wake Yerusalema kwa Hezekia mufalme wa Yuda na kwa watu wote wa inchi ya Yuda waliokuwa Yerusalema, akisema: “Hivi ndivyo Saniharibu mufalme wa Asuria anavyosema: Munategemea nini hata munakaa Yerusalema, muji ambao umezungukwa? Si Hezekia ndiye anayewadanganya mukufe kwa njaa au kiu anapowaambia: ‘Yawe, Mungu wenu atawaokoa toka mikono ya mufalme wa Asuria?’ Si ni huyu Hezekia ndiye aliyeharibu pahali pake pa kuabudia na mazabahu zake na kuwaamuru watu wote wa inchi ya Yuda na Yerusalema akisema: ‘Mutaabudu mbele ya mazabahu moja, na juu yake mutateketeza sadaka zenu?’ Hamujui yale yote ambayo mimi na babu zangu tumewatendea watu wote wa inchi zingine? Miungu ya watu wa inchi hizo iliweza kukomboa inchi zao toka mikono yangu? Ni mungu gani kati ya miungu ya mataifa yale yaliyoharibiwa kabisa na babu zangu aliyeweza kuwakomboa watu wake kutoka katika mikono yangu ndiyo nanyi mukuwe na tumaini kwamba Mungu wenu atawaokoa toka mikono yangu? Musidanganywe na Hezekia wala musishawishiwe kwa hayo. Musimwamini mutu huyu, kwa maana hakujatokea mungu wa taifa au mufalme yeyote aliyeweza kuwakomboa watu wake kutoka mikono ya mufalme wa Asuria. Vile vile mungu wenu hataweza!” Watumishi wa mufalme wa Asuria walisema maneno mengine mengi mabaya juu ya Mungu wetu Yawe na juu ya Hezekia mutumishi wake. Mufalme mwenyewe aliandika barua akamutukana na kumuzarau Yawe, Mungu wa Israeli, akisema: “Kama vile ambavyo miungu ya inchi zingine haikuweza kuwaokoa watu wao kutoka mikono yangu, vile vile mungu wa Hezekia hataweza kuwaokoa watu wake.” Wakubwa wale wakawaambia kwa sauti kubwa kwa luga ya Kiebrania, watu wa Yerusalema waliokuwa juu ya ukuta, wakikusudia kuwatia hofu na woga kusudi wakamate muji. Wakasema juu ya Mungu wa Yerusalema kama vile wangesema juu ya miungu ya mataifa mengine ambayo ni sanamu tu zilizotengenezwa kwa mikono ya wanadamu. Halafu mufalme Hezekia na nabii Isaya, mwana wa Amozi, wakamwomba Mungu na kumulilia awasaidie kwa ajili ya mambo haya. Naye Yawe akatuma malaika aliyewaua waaskari shujaa, majemadari na wakubwa katika kambi ya mufalme wa Asuria. Basi, mufalme wa Asuria akarudia katika inchi yake akijaa haya. Mara tu alipoingia ndani ya nyumba ya mungu wake, wana wake mwenyewe wakamwua palepale kwa upanga. Kwa njia hii basi, Yawe akamwokoa mufalme Hezekia na wakaaji wa Yerusalema kutoka mukono wa Saniharibu mufalme wa Asuria, na kutoka mukono wa waadui zake wote. Akawapa maisha ya amani na wajirani zao wote. Watu wengi sana walikuja wakamuletea Yawe sadaka kule Yerusalema, vilevile wakamuletea Hezekia, mufalme wa Yuda zawadi za bei kali. Hivyo kutoka wakati ule, akasifiwa sana na mataifa mengine yote. Wakati ule, Hezekia akagonjwa sana, karibu kufa. Akamwomba Yawe, naye akamujibu na kumwonyesha kitambulisho. Lakini Hezekia hakumutolea Yawe shukrani kwa yale yote aliyomutendea kwa sababu moyo wake ulikuwa umejaa majivuno. Hii ikasababisha kutaabika kwa inchi ya Yuda na Yerusalema. Kwa hiyo kasirani ikakuwa juu yake, juu ya inchi ya Yuda na juu ya Yerusalema. Kisha Hezekia akanyenyekea akaacha kuwa na moyo uliojaa majivuno, yeye na wakaaji wa Yerusalema wakajinyenyekeza; kwa hiyo kasirani ya Yawe haikuwafikia wakati wa utawala wa Hezekia. Mufalme Hezekia akatajirika sana na kuheshimiwa. Alijitengenezea hazina za feza, za zahabu, za mawe ya bei kali za viungo, ngao na za aina zote za vyombo vya bei kubwa. Vilevile alijijengea nyumba za kuwekea mazao ya ngano, divai na mafuta, na mazizi kwa ajili ya ngombe na mengine kwa ajili ya kondoo. Vile vile alijiongezea miji kwa ajili yake mwenyewe, makundi mengi ya ngombe na kondoo kwa sababu Yawe alimupa mali nyingi. Mufalme Hezekia ndiye aliyefunga maji ya chemichemi ya Gihoni, akayachimbia mufereji na kuyapitisha chini moja kwa moja mpaka upande wa magaribi wa muji wa Daudi. Hezekia alijaliwa katika kila jambo alilofanya, na hata wakati ambapo wajumbe wa wakubwa wa Babeli waliotumwa kwake kuuliza juu ya mambo ya ajabu yaliyotokea mule, Mungu, alimwacha ajiamulie mwenyewe, kusudi amupime na kujua yote yaliyokuwa ndani ya moyo wake. Matendo mengine ya mufalme Hezekia na wema wake, yameandikwa katika “Maono ya nabii Isaya mwana wa Amozi,” katika Kitabu cha Wafalme wa Yuda na Israeli. Hezekia akakufa na kuzikwa kwenye sehemu ya juu ya makaburi ya wafalme. Watu wote wa inchi ya Yuda na wakaaji wa Yerusalema wakamutolea heshima kubwa wakati wa kifo chake, naye Manase, mwana wake, akatawala pahali pake. Manase alikuwa na umri wa miaka kumi na miwili alipoanza kutawala, akatawala kutoka Yerusalema kwa muda wa miaka makumi tano na mitano. Alitenda maovu mbele ya Yawe kwa kuiga mienendo miovu ya mataifa ambayo Yawe aliyafukuza wakati watu wake wa Israeli walipokuwa wanaingia. Kwa maana alijenga tena pahali pa kuabudia miungu mingine palipokuwa pamebomolewa na baba yake Hezekia; akajenga mazabahu za kuabudia Mabali, na kutengeneza sanamu za Ashera. Vilevile, aliabudu jeshi la mbinguni na kulitumikia. Alijenga tena mazabahu katika nyumba ya Yawe pahali ambapo Yawe alikuwa amesema: “Jina langu litaabudiwa milele katika Yerusalema.” Alijenga mazabahu za kuabudia jeshi la mbinguni kwenye viwanja vya nyumba ya Yawe. Na aliwatoa wana wake kama sadaka ya kuteketezwa kwa moto katika bonde la mwana wa Hinomu. Alipiga ramuli, aliaguza na alitumia hirizi; hata alishirikiana na waaguzi wanaosemezana na mizimu na wachawi. Alitenda maovu mengi mbele ya Yawe, akamukasirikisha. Nayo sanamu aliyotengeneza, akaiweka katika nyumba ya Mungu ambayo aliizungumuzia, mbele ya Daudi na mwana wake Solomono: “Katika nyumba hii na katika Yerusalema kati ya makabila kumi na mawili ya Israeli, ndipo pahali nitakapoabudiwa milele. Na ikiwa watu wa Israeli watajali kutenda yote niliyowaamuru, Sheria yote, masharti, na maagizo yaliyotolewa kwa mukono wa Musa, basi sitawaacha hata kidogo wafukuzwe kutoka katika inchi hii ambayo niliwapa babu zao.” Lakini Manase aliwapotosha watu wa inchi ya Yuda na wakaaji wa Yerusalema, wakatenda maovu zaidi kuliko mataifa ambayo Yawe aliyaangamiza mbele ya watu wa Israeli. Yawe akamwonya Manase na watu wake, lakini hawakumusikia. Kwa hiyo, Yawe akawaleta majemadari wa jeshi la mufalme wa Asuria. Hao majemadari wakamukamata Manase kwa ndoana, wakamufunga kikomo cha shaba, wakamupeleka mpaka Babeli. Wakati alipokuwa katika taabu, akamwomba Yawe, Mungu wake rehema. Akajinyenyekeza sana mbele ya Mungu wa babu zake. Alimusihi, naye Mungu akapokea maombi yake na kusihi kwake, akamurudisha Yerusalema katika ufalme wake. Halafu Manase akatambua kwamba Yawe ndiye Mungu. Nyuma ya hayo, Manase akajenga ukuta mwingine upande wa inje wa muji wa Daudi, upande wa magaribi wa Gihoni, katika bonde, akauendelesha mpaka kwenye Mulango wa Samaki, akauzungusha Ofeli; akauinua juu sana. Pamoja na hayo, akaweka majemadari wa majeshi katika miji yote ya inchi ya Yuda yenye kuta. Akatoa katika nyumba ya Yawe miungu yote ya kigeni na sanamu pamoja na mazabahu zote alizokuwa amejenga kwenye mulima wa nyumba ya Yawe na katika Yerusalema; akavitupa inje ya muji. Akarudisha mazabahu ya kumwabudia Yawe, na juu yake akatoa sadaka za amani na za shukrani, akawaamuru watu wa inchi ya Yuda wamwabudu Yawe, Mungu wa Israeli. Hata hivyo watu wakaendelea kutoa sadaka kwenye nafasi ya kufanyia ibada, lakini kwa Yawe, Mungu wao tu. Matendo mengine ya Manase, maombi yake kwa Mungu wake na maneno ya waonaji waliozungumuza naye katika jina la Yawe, Mungu wa Israeli, yote yameandikwa katika Kitabu cha Mambo ya Wafalme wa Israeli. Maombi yake na jinsi Mungu alivyomupokea, zambi zake zote na ukosefu wa uaminifu kwake, pahali alipojenga pa kutambikia na jinsi alivyotengeneza sanamu za Ashera na sanamu zingine mbele ya kujinyenyekeza, vimeandikwa katika Kitabu cha Mambo ya Waonaji. Manase alikufa na kuzikwa katika nyumba yake ya kifalme, naye Amoni, mwana wake, akatawala pahali pake. Amoni alikuwa na umri wa miaka makumi mbili na miwili alipoanza kutawala inchi ya Yuda, alitawala miaka miwili akiwa kule Yerusalema. Alitenda maovu mbele ya Yawe, kama vile baba yake Manase alivyofanya. Vilevile alitoa sadaka na kutumikia sanamu ambazo baba yake Manase alichonga. Naye hakujinyenyekeza mbele za Yawe, kama vile Manase alivyofanya, lakini yeye aliongeza kutenda makosa zaidi. Kisha watumishi wake walimufanyia shauri baya na kumwua katika nyumba yake ya kifalme. Lakini watu wa inchi ya Yuda wakawaua wale wote waliomufanyia Amoni shauri baya, kisha wakamufanya Yosia, mwana wake kuwa mufalme pahali pake. Yosia alikuwa na umri wa miaka minane alipoanza kutawala, alitawala miaka makumi tatu na mumoja akiwa kule Yerusalema. Alitenda kwa usawa mbele ya Yawe. Alifuata njia za Daudi babu yake, na kushika amri za Yawe kwa uangalifu. Katika mwaka wa ine wa utawala wake, mufalme Yosia, akiwa bado kijana, alianza kumwabudu Mungu wa Daudi, babu yake. Kisha alipokuwa na umri wa miaka kumi na miwili alianza kusafisha inchi ya Yuda na Yerusalema kwa kuharibu pahali pa kutambikia miungu mingine, sanamu za Ashera, na sanamu zingine za kuchonga na za kuyeyusha. Watu wake walibomoa mazabahu za ibada za Mabali mbele yake na alikatakata mazabahu za kufukizia ubani zilizoinuliwa juu ya mazabahu hizo; vilevile alipondaponda sanamu za Ashera na zingine za kuchonga na za kuyeyusha; akazifanya kuwa mavumbi, nayo mavumbi akayamwanga juu ya makaburi ya wale ambao walizitolea sadaka. Akateketeza mifupa ya makuhani wa miungu hiyo kwenye mazabahu zao, hivyo akasafisha inchi ya Yuda na Yerusalema. Alifanya vile vile katika miji ya Manase, ya Efuraimu, ya Simeoni mpaka ya Nafutali na kwenye mabomoko yaliyokuwa kandokando ya miji hiyo. Alibomoa mazabahu na kupondaponda Maashera na sanamu za kuchongwa zikakuwa mavumbi. Vilevile akazikatakata mazabahu za kufukizia ubani katika inchi yote ya Israeli. Kisha akarudi Yerusalema. Katika mwaka wa kumi na nane wa utawala wake, wakati ambapo alikuwa amekwisha kuisafisha inchi na nyumba, alituma watu watatu: Safani mwana wa Azalia, Masea liwali wa muji na Yoa mwana wa Yoahazi, mwandishi kusudi waende kutengeneza nyumba ya Yawe, Mungu wake. Wakamwendea Hilkia, Kuhani Mukubwa, wakamupa feza zilizokuwa zimeletwa katika nyumba ya Mungu ambazo zilikusanywa na Walawi walinzi wa mulango, kutoka kwa watu wa Manase, Efuraimu na kutoka pande zingine zote za Israeli, inchi ya Yuda yote na ya Benjamina, na vilevile kutoka kwa wenyeji wa Yerusalema. Zikawekwa katika mikono ya wale wafundi waliosimamia kazi ya kutengeneza nyumba ya Yawe; na wafundi waliofanya kazi katika nyumba ya Yawe wakazitoa kwa kutengeneza na kufanya upya nyumba. Wakawapatia waseremala na wajengaji kwa ajili ya kununua mawe yaliyochongwa, mbao za kuunganishia na nguzo za kutumia kwa kutengeneza yale majengo ambayo wafalme wa inchi ya Yuda waliyobomoa. Watu wale walifanya kazi hiyo kwa uaminifu, wakiwa chini ya uongozi wa Walawi Yahati na Obadia, wa ukoo wa Merari na Zakaria na Mesulamu wa ukoo wa Kohati. Walawi wote waliokuwa na ujuzi sana wa kupiga vyombo vya muziki, waliwasimamia wabebaji wa mizigo na kuwaongoza wote waliofanya kazi mbalimbali, na kati ya Walawi kulikuwa waandishi, wakubwa na hata walinzi wa mulango. Wakati walipokuwa wakitoa inje feza zilizokuwa zimeletwa katika nyumba ya Yawe, kuhani Hilkia akapata kitabu cha Sheria ya Yawe iliyotolewa kwa mukono wa Musa. Kisha Hilkia akamwambia Safani mwandishi: “Nimepata kitabu cha Sheria katika nyumba ya Yawe.” Halafu Hilkia akamupatia Safani kitabu kile. Naye Safani akamupelekea mufalme kitabu kile na kumupasha habari, akisema: “Yote watumishi wako waliyopewa wanayafanya. Wamekusanya feza zilizopatikana katika nyumba ya Yawe, halafu wakazitoa kwa wasimamizi na kwa wafundi.” Kisha mwandishi Safani akamwambia mufalme: “Kuhani Hilkia amenipa kitabu.” Naye Safani akakisoma mbele ya mufalme. Mufalme aliposikia maneno ya Sheria akapasua nguo yake. Halafu mufalme akaamuru Hilkia, Ahikamu mwana wa Safani, Abidoni mwana wa Mika, mwandishi Safani na Asaya, mutumishi wa mufalme, akisema: “Mwende mutafute shauri kutoka kwa Yawe kwa ajili yangu na kwa ajili ya watu ambao wamebaki katika Israeli na Yuda, juu ya maneno yanayokuwa katika kitabu kilichopatikana. Kwa sababu kasirani ya Yawe imetuangukia maana babu zetu hawakushika Neno la Yawe wala kufanya yaliyoandikwa humo.” Kwa hiyo Hilkia pamoja na wale wengine mufalme aliowatuma wakamwendea nabii Hulda muke wa Salumu, mwana wa Tokati, mujukuu wa Hasira, mulinzi wa nguo zilizotumika katika hekalu; (alikuwa anaishi katika Yerusalema katika mukoa wa pili); nao walizungumuza naye juu ya yaliyotokea. Basi akawaambia: “Hivi ndivyo Yawe, Mungu wa Israeli anavyosema: mumwambie yule aliyewatuma kwangu, Yawe anasema hivi: ‘Angalia nitaleta uovu juu ya Yerusalema na juu ya wakaaji wake, laana zote zilizoandikwa katika kitabu kilichosomwa mbele ya mufalme wa Yuda. Kwa sababu wameniacha mimi na kufukizia miungu mingine ubani kusudi wanikasirikishe sana kwa kazi zote za mikono yao, basi kasirani yangu itamwagika juu ya pahali hapa wala haitatulizwa. Lakini juu ya mufalme wa Yuda, aliyewatuma kutafuta shauri la Yawe mumwambie kwamba, hivi ndivyo Yawe, Mungu wa Israeli, anavyosema juu ya maneno uliyoyasikia, kwa sababu umetubu na kunyenyekea mbele yangu, hata umepasua nguo yako na kulia uliposikia maneno yangu juu ya pahali hapa, na juu ya wakaaji wake, na umejinyenyekeza mbele yangu, nami vilevile nimekusikia. –Ni ujumbe wa Yawe.– Azabu ambayo nitailetea Yerusalema, sitaileta wakati ungali muzima. Utawala wako utakuwa wa amani.’ ” Basi wajumbe wakamupelekea mufalme Yosia habari hii. Kisha mufalme Yosia akaita na kukusanya viongozi wote wa inchi ya Yuda na Yerusalema. Naye mufalme akaenda katika nyumba ya Yawe pamoja na wanaume wote wa inchi ya Yuda, na wakaaji wa Yerusalema wakifuatana na makuhani, Walawi na watu wengine wote wakubwa kwa wadogo. Halafu akawasomea maneno ya kitabu cha agano kilichopatikana katika nyumba ya Yawe. Kisha mufalme akasimama kwa pahali pake akafanya agano mbele ya Yawe, kumufuata Yawe, kushika amri, maamuzi na masharti yake kwa moyo wake wote na kwa roho yake yote, kutenda maneno yote ya agano yaliyoandikwa katika kitabu hiki. Tena akawasukuma wote waliokuwa katika Yerusalema na inchi ya Benjamina kushika agano lile. Nao wakaaji wa Yerusalema walitenda kwa kufuata agano la Mungu, Mungu wa babu zao. Kisha Yosia akaondoa sanamu zote za kuchukiza zilizokuwa katika eneo lote la watu wa Israeli, na kuwasukuma watu wote wa Israeli kumutumikia Yawe, Mungu wao. Katika maisha yake yote hawakumwacha Yawe, Mungu wa babu zao. Mufalme Yosia akafanyia Yawe sikukuu ya Pasaka katika Yerusalema, wakachinja wana-kondoo wa Pasaka siku ya kumi na ine ya mwezi wa kwanza. Akawaweka makuhani kwa kazi zao ambazo walihitajika kufanya katika nyumba ya Yawe na kuwatia moyo wazifanye kwa ukamilifu. Pamoja na hayo, akawapa Walawi waliowafundisha watu wa Israeli na ambao walitakaswa kwa ajili ya Yawe, maagizo haya: “Muweke Sanduku takatifu ndani ya nyumba ambayo Solomono mwana wa Daudi, mufalme wa Israeli aliyojenga; hamuhitaji kulibebabeba tena juu ya mabega. Sasa mumutumikie Yawe, Mungu wenu, na watu wake Waisraeli. Mushike kazi yenu kulingana na ukoo zenu, kufuatana na maagizo ya Daudi mufalme wa Israeli na ya Solomono mwana wake. Musimame vilevile Pahali Patakatifu kama vile wasimamizi wa jamaa za ukoo zenu wasiofanya kazi za ukuhani, na kila mumoja asimamie jamaa moja ya Walawi. Muchinje mwana-kondoo wa Pasaka, mujitakase, halafu mutayarishe Pasaka kwa ajili ya wandugu zenu, kusudi waweze kutimiza neno la Yawe lililosemwa na Musa.” Kisha Yosia akawapa watu, wana-mbuzi yapata elfu makumi tatu, na ngombe dume elfu tatu, wote hawa toka katika makundi ya mufalme. Nao wakubwa wake, kwa mapenzi yao, waliwapa watu, makuhani na Walawi. Hilkia, Zakaria na Yehieli, wasimamizi wa nyumba ya Mungu, waliwapa makuhani wana-kondoo na wana-mbuzi elfu mbili mia sita na ngombe dume mia tatu kwa ajili ya sadaka za Pasaka. Naye Konania na wandugu zake wawili, Semaya na Netaneli, pamoja na Hasabia, Yeieli na Yozabadi, waliokuwa viongozi wa Walawi, nao vilevile waliwapa wana-kondoo na wana-mbuzi elfu tano na ngombe dume mia tano, kwa ajili ya sadaka za Pasaka. Basi utaratibu wa kazi ukapangwa, makuhani wakasimama pahali pao, na Walawi katika makundi yao; sawasawa na amri ya mufalme. Wakachinja mwana-kondoo wa Pasaka, nao makuhani wakanyunyiza damu waliyopokea kwa mikono yao nao Walawi wakachuna nyama. Halafu wakatenga sadaka za kuteketeza kwa moto kusudi wapate kuzigawanya kwa watu kulingana na jamaa zao kusudi wamutolee Yawe kama vile ilivyoandikwa katika kitabu cha Musa. Nao wakafanya vile vile na wale ngombe dume. Wakachoma mwana-kondoo wa Pasaka juu ya moto kufuatana na maagizo; vilevile wakatokotesha sadaka takatifu katika vyungu, masufuria na kwenye vikaango, na kuwagawanyia upesiupesi watu wasiofanya kazi ya ukuhani. Kisha, Walawi wakafanya matayarisho kwa ajili yao wenyewe na kwa makuhani kwa maana makuhani wa uzao wa Haruni walikuwa wanashugulika na kutoa sadaka za kuteketeza kwa moto, na vipande vya mafuta, mpaka usiku; kwa hiyo Walawi walitayarisha kwa ajili yao wenyewe na kwa ajili ya makuhani wa uzao wa Haruni. Nao waimbaji wa uzao wa Asafu wakashika nafasi zao, kufuatana na maagizo ya mufalme Daudi, Asafu, Hemani na Yedutuni, nabii wa mufalme. Nao walinzi wa mulango walikuwa kwenye milango; hawakuhitajika kuacha nafasi zao za kazi kwa sababu wandugu zao Walawi waliwatayarishia Pasaka. Hivyo basi, kazi yote ya Yawe ikatayarishwa siku hiyo, kwa kufanya Pasaka na kutoa sadaka za kuteketeza kwenye mazabahu ya Yawe; kama vile mufalme Yosia alivyoamuru. Wakati ule watu wote wa Israeli waliokuwa pale walifanya sikukuu hiyo ya Pasaka na sikukuu ya Mikate Isiyotiwa Chachu, kwa muda wa siku saba. Pasaka kama hiyo ilikuwa haikufanyika katika Israeli yote tangu siku za nabii Samweli. Hakujatokea mufalme hata mumoja wa Israeli aliyefanya Pasaka kama hii iliyofanyika na mufalme Yosia, makuhani, Walawi na watu wote wa inchi ya Yuda, wa Israeli vilevile na wakaaji wa Yerusalema. Pasaka hiyo ilifanyika katika mwaka wa kumi na nane wa utawala wa mufalme Yosia. Nyuma ya haya yote mufalme Yosia aliyofanya kwa ajili ya hekalu, Neko, mufalme wa Misri akapanda kwenda kushambulia Karkemisi kwenye muto Furati. Naye mufalme Yosia akatoka kwa kumushambulia, lakini mufalme Neko akamutumia ujumbe akisema: “Vita hivi havikuelekei wewe hata kidogo, ewe mufalme wa Yuda. Sikukuja kupigana nawe lakini na waadui zangu, na Mungu ameniamuru niharakishe. Acha basi kumupinga Mungu, ambaye yuko upande wangu, kama sivyo atakuangamiza.” Lakini Yosia hakukubali kumwachilia. Akakataa kusikiliza maneno Mungu aliyosema kwa njia ya Neko, kwa hiyo akajibadilisha kusudi asitambulikane, kisha akaingia katika vita katika bonde la Megido. Nao wapiga upinde wakamuchoma mufalme Yosia mishale; basi mufalme akawaambia watumishi wake: “Muniondoshe! Nimeumia vibaya sana.” Basi watumishi wake walipomutoa katika gari lake la vita, wakamubeba na gari lake la pili mpaka Yerusalema. Naye akakufa na kuzikwa katika makaburi ya kifalme. Watu wote wa inchi ya Yuda na Yerusalema wakaomboleza kifo cha Yosia. Nabii Yeremia vilevile akatunga shairi la maombolezo kwa ajili ya kifo chake; nao waimbaji wote, wanaume na wanawake, wanamutaja Yosia katika maombolezo yao, mpaka leo. Wakakusudia kuwa wanafanya maombolezo haya katika Israeli; angalia nayo yameandikwa katika Maombolezo. Matendo mengine ya Yosia na matendo yake mema kama vile yalivyoandikwa katika Sheria ya Yawe, na matendo yake tangu mwanzo mpaka mwisho, angalia yameandikwa katika Kitabu cha Wafalme wa Israeli na Yuda. Watu wa inchi ya Yuda wakatwaa Yoahazi, mwana wa Yosia, wakamuweka kuwa mufalme pahali pa baba yake. Yoahazi alikuwa na umri wa miaka makumi mbili na mitatu alipoanza kutawala; akatawala kwa muda wa miezi mitatu akiwa kule Yerusalema. Kisha mufalme wa Misri akamwondoa kule Yerusalema na kulipisha inchi kodi ya kilo elfu tatu na mia ine za feza na kilo makumi tatu na ine za zahabu. Kisha mufalme wa Misri akamweka Eliakimu, ndugu ya Yoahazi kuwa mufalme wa Yuda na Yerusalema, na akabadilisha jina lake kuwa Yoyakimu; lakini Neko akamupeleka ndugu yake Yoahazi mpaka Misri. Yoyakimu alikuwa na umri wa miaka makumi mbili na mitano alipoanza kutawala, akatawala kwa muda wa miaka kumi na mumoja akiwa kule Yerusalema. Alitenda maovu mbele ya Yawe, Mungu wake. Kisha Nebukadneza mufalme wa Babeli, akamushambulia, akamufunga kwa minyororo kwa kumupeleka Babeli. Nebukadneza akatwaa vilevile vyombo vimoja vya nyumba ya Yawe akavipeleka Babeli na kuviweka katika nyumba ya kifalme kule Babeli. Basi matendo mengine ya Yoyakimu, pamoja na machukizo aliyotenda na mambo mengine yaliyoonekana juu yake yameandikwa katika Kitabu cha Wafalme wa Israeli na Yuda; naye Yoyakini mwana wake akatawala pahali pake. Yoyakini alikuwa na umri wa miaka minane alipoanza kutawala, alitawala kule Yerusalema kwa muda wa miezi mitatu na siku kumi. Alitenda maovu mbele ya Yawe. Mwaka ulipokwisha, mufalme Nebukadneza alituma wajumbe, wakamuchukua Yoyakini na kumupeleka mpaka Babeli, pamoja na vyombo vya bei kali vya nyumba ya Yawe. Akamweka ndugu yake Sedekia kuwa mufalme wa Yuda na Yerusalema. Sedekia alikuwa na umri wa miaka makumi mbili na mumoja alipoanza kutawala, akatawala kule Yerusalema kwa muda wa miaka kumi na mumoja. Alitenda maovu mbele ya Yawe, Mungu wake, wala hakunyenyekea mbele ya nabii Yeremia ambaye alisema maneno yaliyotoka kwa Yawe. Sedekia alimwasi vilevile mufalme Nebukadneza aliyekuwa amemufanya aape kwa jina la Mungu kwamba hatamwasi. Alikuwa mupotovu sana na kufanya moyo mugumu, akakataa kumugeukia Yawe, Mungu wa Israeli. Hata makuhani, viongozi wa inchi ya Yuda pamoja na watu walikosa uaminifu kabisa wakiiga matendo yote ya kuchukiza ya watu wa mataifa mengine; waliichafua nyumba ya Yawe ambayo yeye mwenyewe alikuwa ameitakasa kule Yerusalema. Yawe, Mungu wa babu zao, mara kwa mara alituma kwao wajumbe wake maana alikuwa na huruma kwa watu wake na makao yake. Lakini wao waliendelea kuwachekelea wajumbe wa Mungu, wakayazarau maneno yake na kuwachekelea manabii wake mpaka kwa mwisho kasirani ya Yawe ikawaka juu ya watu wake hata hakukukuwa wa kuwaponyesha. Kwa hiyo, Yawe alimuleta mufalme wa Wakaldea ambaye aliwaangamiza vijana wao kwa upanga hata ndani ya Pahali Patakatifu; wala hakumuhurumia mutu yeyote akuwe kijana au binti, muzee au muzaifu. Wote Yawe aliwatia katika mikono yake. Alitwaa vyombo vyote vya nyumba ya Mungu vikubwa na vidogo na hazina ya nyumba ya Yawe na ya mufalme na wakubwa wake. Alivipeleka vyote mpaka Babeli. Aliichoma moto nyumba ya Mungu, akaubomoa ukuta wa Yerusalema, akazichoma moto nyumba zote za kifalme na kuharibu vyombo vyake vyote vya bei kali. Watu waliookolewa kwenye vita aliwapeleka katika uhamisho Babeli. Kule wakakuwa watumwa wake na wa wazao wake mpaka ufalme wa Persia ulipoinuka kwa nguvu. Na hivyo likatimia neno la Yawe alilosema kwa njia ya nabii Yeremia: “Mpaka inchi imetimiza Sabato zake, haitalimwa siku zote itakapokuwa ukiwa mpaka miaka makumi saba itakapotimia.” Katika mwaka wa kwanza wa utawala wa Kiro mufalme wa Persia, kusudi litimie neno la Yawe alilolisema kwa njia ya nabii Yeremia, Yawe aliamusha nia ya Kiro naye akatoa amri hii katika ufalme wake wote, vilevile alituma habari hizo kwa njia ya maandiko: “Hivi ndivyo anavyosema Kiro mufalme wa Persia: ‘Yawe, Mungu wa mbingu, amenipatia falme zote za ulimwengu, na ameniagiza nimujengee nyumba katika Yerusalema, katika inchi ya Yuda. Basi sasa kila mutu kati yenu, ninyi wote munaokuwa watu wa Yawe, Mungu wake akuwe pamoja naye, na aende.’ ” Katika mwaka wa kwanza wa utawala wa Kiro mufalme wa Persia, Yawe akatimiza neno alilosema kwa njia ya nabii Yeremia. Yawe akaamusha nia ya Kiro mufalme wa Persia, naye akatoa amri hii katika ufalme wake, vilevile amri hiyo ikatolewa kwa maandiko: Hivi ndivyo Kiro mufalme wa Persia anavyosema: Yawe, Mungu wa mbingu, amenipatia falme zote katika ulimwengu na ameniagiza nimujengee nyumba katika Yerusalema, huko Yuda. Basi sasa, kila mutu kati yenu ninyi wote munaokuwa watu wake, Mungu wake akuwe naye na aende katika Yerusalema huko Yuda, na kuijenga upya nyumba ya Yawe, Mungu wa Israeli, Mungu anayeabudiwa kule Yerusalema. Kila mumoja aliyebaki muzima katika uhamisho akitaka kurudi, wajirani zake wamusaidie kwa kumupa feza, zahabu, mali na nyama, pamoja na matoleo ya mapenzi yake kwa ajili ya nyumba ya Mungu kule Yerusalema. Basi, viongozi wa ukoo za makabila ya Yuda na Benjamina wakaondoka, makuhani na Walawi, na kila mutu ambaye Mungu alimupa moyo wa kwenda kujenga upya nyumba ya Yawe, inayokuwa Yerusalema. Wajirani waliwasaidia watu hao kwa kuwapa vyombo vya feza, zahabu, mali, nyama na vitu vingine vya bei kali, mbali na vile vilivyotolewa kwa mapenzi. Mufalme Kiro akawarudishia vyombo ambavyo mufalme Nebukadneza alikuwa amevitwaa kutoka katika nyumba ya Yawe na kuviweka katika nyumba ya miungu yake. Akamupatia Mitiredati, mulinzi wa hazina, vyombo hivyo, naye akavihesabu mbele ya Sesebasari, mutawala wa Yuda. Hii ndiyo hesabu yake: bakuli makumi tatu za zahabu, bakuli elfu moja za feza, vyetezo makumi mbili na tisa, bakuli ndogo za zahabu makumi tatu, bakuli ndogo za feza mia ine na kumi, vyombo vingine elfu moja. Vyombo vyote vya zahabu na feza, pamoja na vitu vingine vilikuwa jumla yake elfu tano mia ine. Vyote hivi, Sesebasari alivibeba mpaka Yerusalema wakati yeye pamoja na watu wengine walipotolewa toka katika uhamisho kule Babeli kwenda Yerusalema. Hawa ndio watu wa majimbo waliotoka katika utumwa ambao Nebukadneza mufalme wa Babeli aliwapeleka wafungwa Babeli, wakarudi katika Yerusalema katika inchi ya Yuda. Kila mutu alirudi katika muji wake. Viongozi wao walikuwa Zerubabeli, Yesua, Nehemia, Seraya, Relaya, Mordekayi, Bilsani, Misipari, Bigwayi, Rehumu na Bana. Hii ndiyo hesabu ya watu wote wa ukoo za Waisraeli waliorudi kutoka katika uhamisho: wa ukoo wa Parosi: elfu mbili mia moja makumi saba na wawili; wa ukoo wa Sefatia: mia tatu makumi saba na wawili; wa ukoo wa Ara: mia saba makumi saba na watano; wa ukoo wa Pahati-Moabu, maana yake wazao wa Yesua na Yoabu: elfu mbili mia nane kumi na wawili; wa ukoo wa Elamu: elfu moja mia mbili makumi tano na wane; wa ukoo wa Zatu: mia tisa makumi ine na watano; wa ukoo wa Zakayi: mia saba na makumi sita; wa ukoo wa Bani: mia sita makumi ine na wawili; wa ukoo wa Bebayi: mia sita makumi mbili na watatu; wa ukoo wa Azgadi: elfu moja mia mbili makumi mbili na wawili; wa ukoo wa Adonikamu: mia sita makumi sita na sita; wa ukoo wa Bigwayi: elfu mbili na makumi tano na sita; wa ukoo wa Adini: mia ine makumi tano na wane, wa ukoo wa Ateri, ndiye Hezekia: makumi kenda na wanane; wa ukoo wa Besayi: mia tatu makumi mbili na watatu; wa ukoo wa Yora: mia moja kumi na wawili; wa ukoo wa Hasumu: mia mbili makumi mbili na watatu; wa ukoo wa Gibari: makumi kenda na watano. Watu wa muji wa Betelehemu: mia moja makumi mbili na watatu; wa muji wa Netofa: makumi tano na sita; wa muji wa Anatoti: mia moja makumi mbili na wanane; wa muji wa Azimaweti: makumi ine na wawili; wa muji wa Kiriati-Yearimu, wa Kefira na wa Beroti: mia saba makumi ine na watatu; wa muji wa Rama na wa Geba: mia sita makumi mbili na mumoja; wa muji wa Mikimasi: mia moja makumi mbili na wawili; wa muji wa Beteli na Ai: mia mbili makumi mbili na watatu; wa muji wa Nebo: makumi tano na wawili; wa muji wa Magibisi: mia moja makumi tano na sita; wa muji wa Elamu wa pili: elfu moja mia mbili makumi tano na wane; wa muji wa Harimu: mia tatu na makumi mbili; wa muji wa Lodi, Hadidi na wa Ono: mia saba makumi mbili na watano; wa muji wa Yeriko: mia tatu makumi ine na watano; wa muji wa Sena: elfu tatu mia sita na makumi tatu. Hii ndiyo jumla ya makuhani waliorudi kutoka katika uhamisho: wa ukoo wa Yedaya waliokuwa wazao wa Yesua: mia tisa makumi saba na watatu; wa ukoo wa Imeri: elfu moja na makumi tano na wawili; wa ukoo wa Pashuri: elfu moja mia mbili makumi ine na saba; wa ukoo wa Harimu: elfu moja na kumi na saba. Walawi wa ukoo wa Yesua na wa Kadimieli, wazao wa Hodavia waliorudi kutoka katika uhamisho walikuwa makumi saba na wane. Waimbaji (wazao wa Asafu), walikuwa mia moja makumi mbili na wanane. Walinzi wa mulango (wazao wa Salumu, wa Ateri, wa Talmoni, wa Akubu, wa Hatita na wa Sobayi), walikuwa mia moja makumi tatu na tisa. Watumishi wote wa hekalu na wazao wa watumishi wa Solomono waliorudi kutoka katika uhamisho walikuwa watu mia tatu makumi kenda na wawili. Watu walirudi kutoka miji hii: Teli-Mela, Teli-Harsa, Kerubu, Adani na Imeri. Lakini hawakuweza kuhakikisha kwamba walikuwa wazao wa Waisraeli. Wao walikuwa watu wa ukoo wa Delaya wa Tobia na wa Nekoda, kwa jumla watu mia sita makumi tano na wawili. Watu wa ukoo hizi za makuhani vilevile walirudi: ukoo wa Habaya, wa Hakosi na wa Barzilayi. Huyo Barzilayi alikuwa ameoa binti ya Barzilayi wa Gileadi, naye vilevile akaitwa Barzilayi. Hao walitafuta ukoo wao katika kitabu cha ukoo, lakini hawakuonekana humo. Kwa hiyo hawakuruhusiwa kushika ukuhani maana walihesabiwa kuwa wachafu. Mutawala akawaambia kwamba hawaruhusiwi kushiriki chakula kitakatifu sana, mpaka kukuwe kuhani atakayeweza kutoa shauri kwa njia Urimu na Tumimu. Watu hao waliotoka katika uhamisho, walipofika kwenye nyumba ya Yawe katika Yerusalema, viongozi wamoja wa ukoo hizo walitoa matoleo ya mapenzi kwa kusaidia ujenzi wa nyumba ya Mungu katika Yerusalema. Walitoa kila mutu kadiri ya uwezo wake kwa ajili ya kazi hii. Jumla ya matoleo hayo ilikuwa kilo mia tano za zahabu, kilo elfu mbili na mia nane za feza na nguo mia moja kwa ajili ya makuhani. Basi, makuhani, Walawi na watu wengine wamoja wakaanza kuishi katika Yerusalema na katika vijiji vyake. Nao waimbaji, walinzi wa hekalu na watumishi wa hekalu wakaanza kuishi katika miji yao; Waisraeli wote wakaishi katika miji yao. Wakati mwezi wa saba ulipofika, na watu wa Israeli wakiwa wamekwisha kukaa katika miji yao, wote wakakusanyika pamoja katika Yerusalema. Yesua mwana wa Yosadaki, pamoja na makuhani wenzake, na Zerubabeli, mwana wa Sealtieli, pamoja na wandugu zake, wakaijenga upya mazabahu ya Mungu wa Israeli, kusudi waweze kumutolea sadaka za kuteketezwa kwa moto kama ilivyoandikwa katika Sheria ya Musa, mutu wa Mungu. Wakaijenga mazabahu hiyo pahali palepale ilipokuwa hapo zamani, kwa kuwa waliwaogopa watu waliokuwa wanaishi katika inchi hiyo. Kisha wakakuwa wanamutolea Yawe sadaka za kuteketezwa kwa moto juu yake kila siku asubui na magaribi. Wakafanya sikukuu ya vibanda kama ilivyoandikwa katika Sheria; kila siku walitoa sadaka za kuteketezwa kwa moto zilizohitajika kwa ajili ya siku hiyo. Walitoa vilevile sadaka za kawaida ambazo ziliteketezwa nzima, sadaka zilizotolewa wakati wa sikukuu ya mwandamo wa mwezi na katika sikukuu nyingine zote alizoagiza Yawe. Vilevile walitoa sadaka zote za mapenzi. Ingawa musingi wa hekalu la Yawe ulikuwa bado kuwekwa, watu walianza kutoa sadaka za kuteketezwa kwa moto tangu siku ya kwanza ya mwezi wa saba. Watu walitoa feza za kuwalipa waseremala na wajengaji, walitoa vilevile chakula, vinywaji na mafuta, kusudi vipelekwe katika miji ya Tiro na Sidona kubadilishwa na miti ya mierezi kutoka Lebanoni. Miti hiyo ililetwa kwa njia ya bahari mpaka Yopa. Haya yote yalifanyika kwa musaada wa mufalme Kiro wa Persia. Basi, watu wakaanza kazi katika mwezi wa pili wa mwaka wa pili nyuma ya kufikia kwenye nyumba ya Mungu katika Yerusalema. Zerubabeli, mwana wa Saltieli, Yesua mwana wa Yosadaki, wandugu zao wengine, makuhani, Walawi na watu wengine wote waliorudi Yerusalema kutoka katika uhamisho, wakajiunga nao katika kazi hiyo. Walawi wote waliokuwa na umri wa miaka makumi mbili au zaidi, walichaguliwa kwa kusimamia kazi ya kuijenga upya nyumba ya Yawe. Yesua, wana wake na jamaa yake, pamoja na Kadimieli na wana wake, (wa ukoo wa Yuda) walishirikiana kwa kusimamia ujenzi wa nyumba ya Mungu. Wakasaidiwa na wazao wa Henadadi na wandugu zao Walawi. Wajengaji walipoanza kuweka musingi wa hekalu la Yawe, makuhani wakiwa wamevaa nguo zao, walisimama pahali pao na baragumu katika mikono, nao Walawi wa ukoo wa Asafu wakisimama na matoazi yao, basi, wakamutukuza Yawe kufuatana na maagizo ya mufalme Daudi wa Israeli. Wakaimba kwa kupokezana, wakimusifu na kumutukuza Yawe: “Yeye ni muzuri, wema wake kwa Waisraeli unadumu milele.” Watu wote walipaza sauti kwa nguvu zao zote, wakamusifu Yawe kwa sababu ya kuanza kujenga musingi wa nyumba ya Yawe. Wengi kati ya makuhani, Walawi, na viongozi wa ukoo waliokuwa wazee na ambao walikuwa wameiona nyumba ya kwanza, wakalia kwa sauti kubwa walipouona musingi wa nyumba hii mupya unawekwa, ingawa watu wengine wengi walipaza sauti kwa furaha. Watu hawakuweza kutofautisha kati ya sauti za furaha na za kilio kwa sababu zilikuwa nyingi na zilisikilika mbali sana. Kisha waadui za watu wa Yuda na Benjamina waliposikia kwamba watu waliorudi kutoka katika uhamisho wanalijenga upya hekalu la Yawe, Mungu wa Israeli, wakamwendea Zerubabeli na viongozi wa ukoo, na kumwambia: “Tafazali tushirikiane katika ujenzi wa hekalu. Sisi kama vile ninyi tunamwabudu Mungu wenu, na tumekuwa tukimutolea sadaka tangu zamani za Esari-Hadoni, mufalme wa Asuria aliyetuleta hapa.” Lakini Zerubabeli, Yesua na viongozi wengine wa ukoo za Waisraeli wakawaambia: “Sisi hatuhitaji musaada wowote kutoka kwenu kwa kuijenga nyumba ya Mungu wetu. Sisi wenyewe tutamujengea Yawe, Mungu wa Israeli, kama vile mufalme Kiro wa Persia alivyotuamuru.” Hapo, watu waliokuwa wanaishi pahali pale wakaanza kuwavunja moyo na kuwatisha Wayuda kusudi wasiendelee kama walivyokusudia. Tena wakawalipa wakubwa wa serikali ya Persia kituliro kusudi wapinge kazi ya Wayuda. Wakaendelea kufanya hivyo muda wote wa utawala wa Kiro, mpaka wakati wa utawala wa Dario. Kwa mwanzo wa utawala wa mufalme Ahasuero, waadui za watu waliokaa Yuda na Yerusalema wakaandika mashitaki juu yao. Tena wakati wa utawala wa Artasasta, mufalme wa Persia, Bisilamu, Mitiredati, Tabeli na warafiki zao, wakamwandikia barua mufalme Artasasta. Barua hiyo iliandikwa katika herufi za Kiaramea na kutafsiriwa. Vilevile mutawala Rehumu na Simusayi, karani wa jimbo, wakamwandikia Artasasta barua hii juu ya Yerusalema: Hii barua inatoka kwa mutawala Rehumu na kwa Simusayi, karani wa jimbo pamoja na wenzetu, na waamuzi, wakubwa wote ambao pale mbele walitoka Ereki, Babeli, Susani, Dini, Afarsati, Terpeli, Deha na Elamu, pamoja na watu wa mataifa mengine ambao Asurbanipali, mutu mukubwa na mwenye nguvu akawahamisha na kuwaweka katika muji wa Samaria na pahali pengine katika jimbo la upande wa magaribi wa muto Furati. Kwa mufalme Artasasta: Sisi watumishi wako katika jimbo la upande wa magaribi wa muto Furati, tunakutumia salamu. Tungependa ufahamu, ewe mufalme, kwamba Wayuda waliokuja hapa kutoka maeneo mengine ya ufalme wako wamekwenda Yerusalema na wanaujenga upya muji huo wa waasi na waovu. Wanamalizia kujenga kuta zake na kutengeneza musingi. Tungependa ufahamu, ewe mufalme, kwamba muji huu ukijengwa upya na kuta zake zikimalizika, watu hawatalipa kodi, malipo ya kuvuka mipaka, na mengine mbalimbali na hazina yako itapunguka. Sasa, kwa sababu ni mapaswa yetu ee mufalme, hatungependa kuona ukivunjiwa heshima, ndiyo maana tumeona ni vizuri tukuarifu kusudi ufanye uchunguzi katika kitabu cha habari za babu zako. Humo utagundua kwamba tangu zamani, muji huu ulikuwa wa waasi na umewasumbua sana wafalme na watawala wa majimbo, na kuwa tangu zamani watu wake ni wachochezi sana; ndiyo sababu muji huo uliangamizwa. Kwa hiyo tunakujulisha kwamba ikiwa muji huu utajengwa upya na kuta zake zikimalizika, hautaweza kutawala jimbo la upande wa magaribi wa muto Furati. Kisha mufalme akatuma jibu hili: Kwa mutawala Rehumu, kwa Simusayi, karani wa jimbo, pamoja na wenzenu wote wanaoishi Samaria na pahali pengine katika jimbo la upande wa magaribi wa muto Furati. Barua muliyonitumia imetafsiriwa na kusomwa mbele yangu. Nimetoa amri uchunguzi ufanyike na imegunduliwa kuwa ni kweli kwamba tangu zamani muji huu wa Yerusalema umekuwa ukiwapinga wafalme na kwamba watu wake wamekuwa waasi na wachochezi wakubwa. Wafalme wenye nguvu wamepata kuutawala muji ule pamoja na jimbo la upande wa magaribi wa Furati wakilipisha kodi, malipo ya kuvuka mipaka na mengine. Kwa hiyo, mutoe amri watu hao waache kuujenga upya muji ule mpaka pale nitakapotoa maagizo mengine. Tena, muangalie sana musichelewe kufanya hivyo, kusudi nisipate hasara. Mara tu waliposomewa barua hii kutoka kwa Artasasta, Rehumu, karani Simusayi na wenzao wakaharakisha kwenda Yerusalema na kuwalazimisha kwa nguvu Wayuda waache kuujenga muji. Kazi ya kuijenga upya nyumba ya Mungu katika Yerusalema ilisimama, na hali hiyo ikaendelea mpaka mwaka wa pili wa utawala wa Dario, mufalme wa Persia. Wakati ule, manabii wawili, Hagai na Zakaria mwana wa Ido, wakawatolea unabii Wayuda waliokuwa wanakaa Yuda na Yerusalema, katika jina la Mungu wa Israeli. Nao Zerubabeli mwana wa Saltieli, na Yesua mwana wa Yosadaki, walipousikia ujumbe huo wakaanza tena kuijenga nyumba ya Mungu katika Yerusalema, wakisaidiwa na manabii wa Mungu. Kisha Tatenayi, mutawala wa jimbo la upande wa magaribi wa muto Furati, Setari-Bozenayi na wenzao, wakakwenda Yerusalema na kuuliza: “Nani aliyewaamuru kuijenga nyumba hii mpaka kuimaliza?” Tena wakauliza: “Ni nani wanaojenga nyumba hii? Tunataka majina yao.” Lakini Mungu alikuwa anawalinda viongozi wa Wayuda, kwa hiyo wakubwa hao hawakuwakataza mpaka pale walipomwandikia mufalme Dario na kupata maoni yake. Basi, Tatenayi, mutawala wa jimbo la upande wa magaribi wa muto Furati, Setari-Bozenayi na wenzao, wakamwandikia mufalme Dario. Walimutumia mufalme barua iliyoandikwa hivi: Kwa mufalme Dario, tunakutakia amani. Tungetaka kukufahamisha, ee mufalme, kwamba tulikwenda katika jimbo la Yuda kunapokuwa nyumba ya Mungu Mukubwa. Nyumba hii inajengwa upya kwa mawe makubwamakubwa na kuta zake zinawekwa nguzo za miti. Kazi hiyo inafanywa kwa uangalifu mukubwa na inaendelea vizuri sana. Tuliwauliza viongozi hao watuambie ni nani aliyewapa amri ya kuijenga upya nyumba hii mpaka kuimaliza. Tukawauliza vilevile majina yao kusudi tuweze kukujulisha wale wanaoongoza kazi hiyo. Wao wakatujibu hivi: “Sisi ni watumishi wa Mungu wa mbingu na dunia, na tunaijenga upya nyumba ambayo ilikuwa imejengwa na kumalizika pale mbele na mufalme mumoja mukubwa wa Israeli.” Lakini kwa sababu babu zetu walimukasirikisha Mungu wa mbingu, yeye akawatia katika mikono ya mufalme Nebukadneza wa Babeli, Mukaldea, aliyeharibu nyumba hii na kuwapeleka watu katika uhamisho kule Babeli. Lakini katika mwaka wa kwanza wa utawala wa mufalme Kiro wa Babeli akatoa amri kwamba nyumba hii ya Mungu ijengwe upya. Vilevile akavirudisha vyombo vya zahabu na feza ambavyo mufalme Nebukadneza alikuwa amevipeleka kutoka katika hekalu kule Yerusalema na kuviweka katika hekalu la Babeli. Vyombo hivyo Kiro akaviondoa toka hekalu la Babeli na kuvipatia Sesebasari ambaye alikuwa amemuchagua akuwe mutawala wa Yuda; akamwamuru akisema: “Utwae vyombo hivyo na kuvirudisha katika hekalu la Yerusalema, na kuijenga upya nyumba ya Mungu pahali pake.” Kisha Sesebasari akakuja na kuweka musingi wa nyumba ya Mungu katika Yerusalema, na tangu wakati huo ujenzi umekuwa ukiendelea mpaka sasa, lakini bado haujamalizika. Basi, ikikupendeza, ewe mufalme, amuru uchunguzi ufanyike katika kitabu cha habari za kifalme katika muji wa Bebeli kama mufalme Kiro alitoa amri nyumba hii ya Mungu ijengwe upya katika Yerusalema. Kisha, tunakuomba utujulishe maoni yako juu ya jambo hili. Mufalme Dario alitoa amri na uchunguzi ukafanywa katika muji wa Babeli katika nyumba ya kuwekea maandiko ya zamani ya kifalme. Lakini kitabu kikapatikana katika muji wa Akimeta katika jimbo la Media, nacho kilikuwa na maagizo haya: “Katika mwaka wa kwanza wa utawala wake, mufalme Kiro alitoa amri kwamba nyumba ya Mungu ijengwe upya katika Yerusalema, na ikuwe pahali pa kutolea sadaka na sadaka za kuteketezwa kwa moto. Urefu wake kwenda juu utakuwa metre makumi mbili na saba na upana wake metre makumi mbili na saba. Kuta zake zitajengwa kwa mustari mumoja wa miti juu ya kila mistari tatu ya mawe makubwa. Mali itakayotumiwa kwa kazi ile itatoka katika hazina ya mufalme. Vilevile, vyombo vyote vya zahabu na feza ambavyo mufalme Nebukadneza alivileta Babeli kutoka katika hekalu la Yerusalema, vitarudishwa na kuwekwa kila kimoja pahali pake katika nyumba ya Mungu.” Halafu Dario akatuma ujumbe huu: Kwa Tatenayi, mutawala wa jimbo la upande wa magaribi wa muto Furati, Setari-Bozenayi na wakubwa wenzako katika jimbo. Musiende kule kwenye hekalu, na muache kazi ya ujenzi wa nyumba hii ya Mungu iendelee. Muache mutawala wa Yuda na viongozi wa Wayuda waijenge nyumba ya Mungu pahali pake. Zaidi ya hayo, ninatoa amri kwamba ninyi mutawasaidia katika kazi hiyo. Mali zao zote walizotumia zitalipwa bila kuchelewa kutoka katika hazina ya mufalme inayotokana na kodi kutoka katika jimbo la upande wa magaribi wa muto Furati. Kila siku, tena bila kukosa, mutawapa makuhani wa Yerusalema kila kitu watakachohitaji; ikuwe ni ngombe dume, wana-ngombe, kondoo dume au wana-kondoo wa sadaka za kuteketezwa kwa moto kwa ajili ya Mungu wa mbinguni, au ngano, chumvi, divai au mafuta. Haya yote yatatendeka kusudi waweze kumutolea Mungu wa mbinguni sadaka zinazomupendeza na waombee maisha yangu mimi mufalme na watoto wangu. Ninaamuru vilevile kwamba mutu yeyote ambaye hatatii amri hii, muti mumoja uongolewe kutoka katika nyumba yake na atundikwe juu yake. Tena, nyumba yake ifanywe kuwa yalala. Mungu aliyeuchagua Yerusalema kuwa pahali pake pa kuabudiwa amwangushe mufalme au taifa lolote litakalopinga amri hii au kutaka kuiharibu nyumba hii ya Mungu inayokuwa katika Yerusalema. Ni mimi Dario niliyetoa amri hii na inapaswa kushikwa. Basi, Tatenayi, mutawala wa jimbo la upande wa magaribi wa muto Furati, Setari-Bozenayi, na wakubwa wenzao, wakafanya bidii kwa kutimiza maagizo ya mufalme. Viongozi wa Wayuda waliendelea vizuri sana na kazi ya ujenzi wa hekalu, wakitiwa moyo na nabii Hagai na Zakaria mwana wa Ido. Wakamaliza ujenzi wa hekalu kama walivyoamriwa na Mungu wa Israeli, na kama walivyoagizwa na mufalme Kiro, mufalme Dario na mufalme Artasasta, wa Persia. Ujenzi wa nyumba hiyo ukamalizika katika siku ya tatu ya mwezi wa Adari, katika mwaka wa sita wa utawala wa mufalme Dario. Basi, watu wa Israeli, makuhani, Walawi na watu wengine waliokuwa wamerudi kutoka katika uhamisho wakaizindua nyumba ya Mungu kwa shangwe kubwa. Wakati wa kuizindua nyumba ya Mungu, walitoa ngombe dume mia moja, kondoo dume mia mbili, wana-kondoo mia ine na beberu kumi na wawili kwa ajili ya sadaka ya kusamehewa zambi, mbuzi mumoja kwa kila kabila la Israeli. Vilevile, kwa ajili ya kazi ya Mungu katika Yerusalema, waliwapanga makuhani katika makundi yao ya Walawi katika zamu zao kufuatana na maagizo yaliyoandikiwa katika kitabu cha Musa. Katika siku ya kumi na ine ya mwezi wa kwanza, watu waliokuwa wamerudi kutoka katika uhamisho walisherehekea Pasaka. Makuhani na Walawi walikuwa wamejitakasa, wote walikuwa safi kabisa. Wakachinja mwana-kondoo wa Pasaka kwa ajili ya watu wote waliorudi kutoka katika uhamisho, wandugu zao makuhani na kwa ajili yao wenyewe. Waliokula mwana-kondoo wa Pasaka walikuwa Waisraeli wote waliorudi kutoka katika uhamisho pamoja na watu wengine wote ambao walikuwa wameziacha njia za mataifa mengine kwa kumwabudu Yawe, Mungu wa Israeli. Kwa muda wa siku saba watu walisherehekea kwa furaha sikukuu ya Mikate Isiyotiwa Chachu; kwa sababu Yawe aliwajalia furaha na kumupa mufalme wa Asuria moyo wa upendo kwao, akawasaidia katika kazi za ujenzi wa nyumba ya Mungu, wa Israeli. Nyuma ya mambo yale, wakati wa utawala wa mufalme Artasasta wa Persia, kulikuwa mutu mumoja aliyeitwa Ezra. Ezra alikuwa mwana wa Seraya mwana wa Azaria mwana wa Hilkia mwana wa Salumu mwana wa Zadoki mwana wa Ahitubu mwana wa Amaria mwana wa Azaria mwana wa Merayoti mwana wa Zerahia mwana wa Usi mwana wa Buki mwana wa Abisua mwana wa Finehasi mwana wa Eleazari mwana wa Haruni, Kuhani Mukubwa. Ezra akaondoka Babeli, yeye alikuwa mwandishi mwenye ujuzi mwingi sana katika Sheria ambayo Yawe, Mungu wa Israeli, alikuwa amemupatia Musa. Na kwa musaada wa Yawe, Mungu wake, mufalme alimupatia Ezra kila kitu alichohitaji. Katika mwaka wa saba wa utawala wa mufalme Artasasta, Ezra akafunga safari kutoka Babeli kwenda Yerusalema. Alikwenda pamoja na watu wamoja wa Israeli, makuhani, Walawi, waimbaji, walinzi wa milango na watumishi wa hekalu. Wakafika Yerusalema katika siku ya kwanza ya mwezi wa tano katika mwaka wa saba wa utawala wa mufalme Artasasta. Yawe akaifanikisha sana safari yao waliyokuwa wameianza siku ya kwanza ya mwezi wa kwanza. Ezra alikuwa amejitoa kwa moyo wote kujifunza Sheria ya Yawe, kuitii na kuwafundisha watu wa Israeli masharti na maagizo zake. Huu ndio mufano wa barua ambayo Artasasta alimupa Ezra, kuhani na mwandishi, na mwenye ujuzi katika amri na masharti ambayo Yawe aliwapa watu wa Israeli. Mimi Artasasta, mufalme wa wafalme, ninatuma barua hii kwa Ezra, kuhani na mutu mwenye ujuzi katika Sheria ya Mungu wa mbinguni. Ninaamuru kwamba katika utawala wangu, Mwisraeli yeyote, au kuhani wao, au Mulawi, akitaka kurudi Yerusalema kwa mapenzi yake, anaweza kwenda pamoja nawe. Mimi pamoja na washauri wangu saba, tunakutuma uende ufanye uchunguzi kule Yuda na Yerusalema kuona kama Sheria ya Mungu wako ambayo umepewa inafuatwa kikamilifu. Utatwaa feza na zahabu ambayo mimi na washauri wangu tumemutolea kwa utashi wetu Mungu wa Israeli ambaye hekalu lake liko katika muji Yerusalema. Utatwaa vilevile feza na zahabu yote utakayokusanya katika jimbo lote la Babeli, pamoja na matoleo ya mapenzi Waisraeli na makuhani wao waliyotoa kwa ajili ya nyumba ya Mungu wao inayokuwa Yerusalema. Feza hiyo utaitumia kwa uangalifu sana kwa kununua ngombe dume, kondoo dume, wana-kondoo na sadaka ya unga na divai, na kuvitoa kwenye mazabahu katika nyumba ya Mungu wenu inayokuwa Yerusalema. Feza na zahabu itakayobaki unaweza kuitumia pamoja na wanainchi wenzako kama vile mutakavyopenda, kufuatana na mapenzi ya Mungu. Vyombo ambavyo umepewa kwa ajili ya ibada ya nyumba ya Mungu wako, utamutolea Mungu wa Yerusalema. Ukihitaji kitu kingine chochote kwa ajili ya nyumba ya Mungu wako unaweza kukipata kutoka katika hazina ya mufalme. Mimi mufalme Artasasta, ninatoa amri kwa walinzi wa hazina wote katika jimbo la upande wa magaribi wa muto Furati kwamba kitu chochote Ezra atakachohitaji, kuhani na mwandishi wa Sheria ya Mungu wa mbinguni, mutamupa, tena bila kusita, feza kiasi anachotaka mpaka kufikia kilo elfu tatu mia ine, ngano kilo elfu kumi, divai litre elfu mbili, mafuta litre elfu mbili, na chumvi kiasi chochote atakachohitaji. Kila kitu Mungu wa mbinguni alichoagiza kwa ajili ya nyumba yake, kinapaswa kutimizwa kikamilifu, kusudi asipate kukasirikia ufalme wangu au wana wangu. Tunawafahamisha tena kwamba inakatazwa kuwadai kodi ya mapato, malipo ya kuvuka mupaka na mengine makuhani, Walawi, waimbaji, walinzi wa mulango, wafanyakazi au watumishi wengine wa nyumba hii ya Mungu. Nawe Ezra, kwa kutumia hekima Mungu wako aliyokupa, hiyo unayokuwa nayo, chagua wanasheria, na waamuzi watakaowaongoza wakaaji wote wa jimbo la upande wa magaribi wa muto Furati ambao wanaishi kufuatana na Sheria ya Mungu wako. Na yule ambaye haijui Sheria hiyo, umufundishe. Mutu yeyote ambaye hatatii Sheria ya Mungu wako na ya mufalme, ahukumiwe mara moja: kufa, kuhamishwa, kunyanganywa mali yake au kufungwa. Ezra akasema: “Asifiwe Yawe, Mungu wa babu zetu, ambaye amemupatia mufalme moyo wa kupamba nyumba ya Yawe inayokuwa Yerusalema. Kwa wema wa Mungu, nimepata musaada wa mufalme na wakubwa wake wenye uwezo mukubwa. Nilipata nguvu kwa sababu Yawe, Mungu wangu, alikuwa pamoja nami, hata nikawakusanya viongozi wa Israeli kusudi warudi pamoja nami.” Nikawakusanya pamoja watu wote pembeni ya muto unaoelekea muji wa Ahava. Kule, tukapiga kambi kwa muda wa siku tatu. Nikaangalia kati ya watu wote pamoja na makuhani, lakini sikupata Walawi kati yao. Nikaita viongozi tisa wakuje kwangu: Eliezeri, Arieli, Semaya, Elnatani, Yaribu, Elnatani, Natani, Zekaria na Mesulamu, pamoja na waalimu wawili, Yoyaribu na Elnatani. Nikawatuma kwa Ido, kiongozi wa jamii ya watu kule Kasifia, nikimwomba yeye pamoja na wenzake watumishi wa nyumba ya Mungu, watuletee watu watakaotumika katika nyumba ya Mungu. Kwa neema ya Mungu, wakatuletea Serebia, mutu mwenye akili na Mulawi wa ukoo wa Mali, pamoja na wana wake na wandugu zake kumi na wanane. Wakatuletea vilevile Hasabia na Yesaya, wote wa ukoo wa Merari, pamoja na wandugu zao makumi mbili. Zaidi ya hao, kulikuwa watumishi wa hekalu mia mbili makumi mbili ambao babu zao walikuwa wamechaguliwa na mufalme Daudi na wakubwa wake kwa kuwasaidia Walawi. Majina ya watu wote hawa yameandikwa. Kisha, nikatoa maagizo kuwa sisi wote tufike karibu na muto Ahara kusudi tufunge kula chakula na kujinyenyekeza mbele ya Mungu wetu na kumwomba atulinde na kutuongoza katika safari yetu pamoja na watoto wetu. Ingekuwa haya kubwa kwangu kumwomba mufalme kundi la waaskari na waaskari wapanda-farasi wa kutulinda na waadui katika njia maana nilikuwa nimekwisha kumwambia kwamba Mungu wetu anawabariki wote wanaomutafuta, lakini anawachukia na kuwaazibu wote wanaomwacha. Kwa hiyo tukafunga na kumwomba Mungu atulinde, naye akayasikia maombi yetu. Halafu kati ya makuhani waliokuwa viongozi nikachagua kumi na wawili: Serebia, Hasabia pamoja na wenzao kumi. Hawa nikawapimia kwa mizani feza, zahabu na vyombo ambavyo mufalme, washauri wake, wakubwa wake pamoja na watu wa Israeli walivyokuwa wamevitoa kwa ajili ya sadaka ya nyumba ya Mungu wetu. Hivi ndivyo vitu nilivyowapimia: feza toni makumi mbili na mbili, vyombo mia moja vya feza, uzito wake kilo makumi saba, zahabu kilo elfu tatu na mia ine, mabakuli makumi mbili ya zahabu, uzito wake kilo nane, vyombo viwili vya shaba nzuri iliyongaa yenye bei kama ya zahabu. Kisha nikawaambia: “Ninyi mumetakaswa mbele ya Yawe. Vilevile na vyombo vimetakaswa na feza na zahabu ni matoleo ya mapenzi kwa Yawe, Mungu wa babu zenu. Tafazali muvilinde na muvitunze mpaka mutakapovipima mbele ya makuhani wakubwa, Walawi na viongozi wa ukoo za Israeli, kule Yerusalema katika vyumba vya nyumba ya Yawe.” Basi, makuhani na Walawi wakatwaa feza, zahabu na vyombo vyote walivyopimiwa, kwa kuvipeleka katika Yerusalema ndani ya nyumba ya Mungu wetu. Katika siku ya kumi na mbili ya mwezi wa kwanza, tukasafiri kutokea kwenye muto Ahava, kwenda Yerusalema. Mungu wetu alikuwa pamoja nasi, akatulinda na waadui na washambulizi katika njia. Tulipofika Yerusalema, tukapumzika kwa muda wa siku tatu. Katika siku ya ine, tukiwa ndani ya nyumba ya Mungu wetu, tukapima ile feza, zahabu na vile vyombo, kisha tukavipatia kuhani Meremoti mwana wa Uria. Meremoti alikuwa pamoja na Eleazari mwana wa Finehasi, na Walawi wawili, Yozabadi mwana wa Yesua, na Noadia mwana wa Binui. Kila kitu kilihesabiwa na kupimwa na wakati huo uzito wa kila kitu uliandikwa. Kisha, watu wote waliorudi kutoka katika uhamisho wakamutolea Mungu wa Israeli sadaka zao za kuteketezwa kwa moto. Wakatoa ngombe dume kumi na wawili kwa ajili ya Israeli yote, kondoo dume makumi kenda na sita na wana-kondoo makumi saba na saba; vilevile walitoa mbuzi kumi na wawili kama sadaka ya kusamehewa zambi. Nyama wote hawa walitolewa kuwa sadaka ya kuteketezwa kwa Yawe. Vilevile wakawapa wasimamizi wa mufalme na watawala wa mukoa wa majimbo ya upande wa magaribi wa muto Furati maagizo waliyopewa na mufalme, nao wakatoa musaada kwa watu na kwa ajili ya nyumba ya Mungu. Nyuma ya mambo haya yote kutendeka, viongozi wakanifikia na kunipa habari hii: “Watu wa Israeli, makuhani na Walawi hawakujitenga na wakaaji wa inchi ambao wanatenda machukizo: Waamoni, Wamoabu na Wamisri, Wakanana, Wahiti, Waperizi, Wayebusi na Waamori. Wayuda wanaoa wanawake wa kigeni na kuwaoea wana wao vilevile. Hivyo, taifa takatifu la Mungu limechanganyika na watu wa mataifa mengine. Vilevile wasimamizi na wakubwa ndio wa kwanza kutenda maovu hayo.” Nilipoyasikia maelezo hayo, nikapasua nguo zangu na koti langu, nikaongoa nywele zangu na ndevu zangu kwa huzuni kubwa na kuikaa chini na kufazaika. Halafu watu wote walioshikwa na hofu kwa sababu ya maneno Mungu wa Israeli aliyosema juu ya makosa ya wale waliorudi kutoka katika uhamisho wakaanza kukusanyika karibu nami nikiwa mwenye kufazaika mpaka magaribi, wakati wa kutoa sadaka. Magaribi, wakati wa kutoa sadaka ulipofika, nikasimama pahali pale nilipokuwa nimeikaa kwa huzuni nazo nguo zangu zimepasuka pamoja na koti, nikapiga magoti na kunyoosha mikono yangu kwa Yawe, Mungu wangu, na kuomba, nikisema: “Ee Mungu wangu, ninaona haya kubwa sana kukiinua kichwa changu mbele yako. Zambi zetu zimelundikana kupita hata vichwa vyetu; makosa yetu yanafika hata mbinguni. Tangu nyakati za babu zetu mpaka sasa, sisi watu wako tumekukosea sana. Na kwa sababu ya zambi zetu, sisi, wafalme wetu na makuhani wetu tulitiwa katika mikono ya wafalme wa inchi za kigeni, tukauawa, tukapelekwa kuwa wafungwa na kunyanganywa mali zetu. Na hata hivi leo, tumetiwa haya kupita kiasi. Lakini sasa, ee Yawe, Mungu wetu, kwa muda mufupi umetuonyesha huruma yako na kuwawezesha wamoja kati yetu kuponyoka kutoka katika utumwa na kuishi kwa usalama pahali pako patakatifu. Pahali pa utumwa, umetupa furaha na maisha mapya. Haukutuacha tuishi katika utumwa ingawa tulikuwa watumwa. Uliwafanya wafalme wa Persia wakuwe wema kwetu na kuturuhusu tuishi na kuijenga nyumba yako iliyokuwa imebomoka, na ukatufanya tukae salama hapa Yuda na Yerusalema. “Lakini sasa, ee Mungu wetu, tuseme nini nyuma ya hayo yote? Maana, tumeziasi amri zako ulizotupa kwa njia ya watumishi wako manabii ukisema: ‘Inchi munayoiendea na ambayo itakuwa mali yenu ni inchi chafu, yenye uchafu wa wakaaji toka inchi mbalimbali, kwa machukizo yao, wameijaza uchafu tele, kila nafasi. Kwa hiyo, musiwaoeshe na wabinti zenu kwa watu hao, wala musiwaruhusu wana wenu kuwaoa wabinti zao. Pia, musishugulikie usalama au mafanikio yao, kusudi ninyi wenyewe mupate kuwa na nguvu, na mufaidie mema ya inchi hiyo na kuwaachia watoto wenu kama vile urizi milele.’ Hata nyuma ya yote yaliyotupata kwa sababu ya maovu yetu na makosa yetu mengi, tunajua kwamba azabu uliyotupa, ee Mungu wetu, ni ndogo ikilinganishwa na makosa yetu, na umewaacha wazima wamoja kati yetu. Tutavunja amri zako tena na kuoana na watu hawa wanaotenda maovu haya? Hautatukasirikia na kutuangamiza kabisa, na kusibaki hata mumoja wetu muzima wala yeyote wa kutoroka? Ee Yawe, Mungu wa Israeli, wewe ni mwenye haki na umetuacha tubaki kama vile tunavyokuwa hivi leo. Tunaungama makosa yetu mbele yako, tukijua kwamba hakuna anayekuwa na haki yoyote ya kuja mbele yako kwa ajili ya makosa haya.” Wakati Ezra alipokuwa anaomba na kuungama naye akilia na kujiangusha uso mpaka chini mbele ya nyumba ya Mungu, kundi kubwa la watu wa Israeli, wanaume, wanawake na watoto, wakakusanyika karibu naye wakilia kwa uchungu mwingi. Halafu Sekania mwana wa Yehieli, wa ukoo wa Elamu, akamwambia Ezra: “Tumekosa uaminifu kwa Mungu kwa kuoa wanawake wa kigeni wa inchi hii, lakini hata hivyo bado kuna tumaini kwa ajili ya Israeli. Kwa hiyo, tufanye agano na Mungu wetu, tuachane na wanawake hawa pamoja na watoto wao, kwa kufuatana na shauri lako na la wengine wanaotii amri za Mungu. Yote yatendeke kwa kufuatana na Sheria. Amuka utende, sisi tutakuunga mukono. Kwa hiyo ujipe moyo ufanye hivyo.” Ezra akasimama na kuanza kuwaapiza makuhani, viongozi, Walawi na Waisraeli wengine wote kwamba watafanya kama ilivyosemwa, nao wakakubali kufanya kiapo. Kisha, Ezra akaondoka mbele ya nyumba ya Mungu, akaenda kwa nyumba ya Yehohanani mwana wa Eliasibu. Kule, Ezra akalala usiku kucha bila kula wala kunywa maji, kwa huzuni aliyokuwa nayo juu ya ukosefu wa imani ya watu waliotoka katika uhamisho. Tangazo likatolewa kila pahali katika inchi ya Yuda na Yerusalema kwa wote waliotoka katika uhamisho kwamba wakusanyike Yerusalema. Ikiwa mutu yeyote atashindwa kufika katika muda wa siku tatu, kulingana na amri iliyotolewa na viongozi, mali yake yote itanyanganywa, naye mwenyewe atatengwa mbali na makutano na jamii ya watu waliorudi kutoka katika uhamisho. Katika siku hizo tatu, kwa siku ya makumi mbili ya mwezi wa tisa, watu wote walioishi katika majimbo ya Yuda na Benjamina wakafika Yerusalema na kukusanyika katika kiwanja cha nyumba ya Mungu. Watu wote walikuwa wakitetemeka kwa sababu ya shauri waliloitiwa na kwa ajili ya mvua nyingi iliyokuwa ikinyesha. Kuhani Ezra akasimama kwa kuzungumuza na watu, akawaambia: “Hamukukuwa waaminifu kwa kuoa wanawake wa kigeni, na hivyo mumeiongezea Israeli kosa. Sasa, mutubu zambi zenu mbele ya Yawe, Mungu wa babu zenu, na kufanya yale yanayomupendeza. Mujitenge na wakaaji wa inchi hii na kuwaacha wake zenu wa kigeni.” Watu wote wakasema kwa sauti na kujibu kwa pamoja: “Ni sawa! Tunapaswa kufanya kama vile unavyosema.” Lakini wakaongeza kusema: “Watu ni wengi na mvua inanyesha sana. Hatuwezi kuendelea kusimama hapa katika kiwanja, na hili si jambo ambalo litamalizika kwa siku moja au mbili! Tumefanya kosa kubwa sana juu ya shauri hili. Afazali wakubwa wetu wabaki Yerusalema kushugulikia jambo hili kwa ajili ya watu wote. Kisha, kila mumoja ambaye ameoa mwanamuke wa kigeni akuje kwa zamu pamoja na viongozi na waamuzi wa muji wake, mpaka pale kasirani kali ya Mungu wetu itakapoondolewa kwetu.” Hakuna aliyepinga mupango huu, isipokuwa tu Yonatani mwana wa Asaeli na Yazeya mwana wa Tikwa, nao wakaungwa mukono na Mesulamu na Mulawi Sabetayi. Watu wote waliorudi kutoka katika uhamisho wakakubali mupango huo, kwa hiyo kuhani Ezra akawachagua wanaume kati ya viongozi wa ukoo mbalimbali na kuyaandika majina yao. Kwa siku ya kwanza ya mwezi wa kumi, watu hao wakaanza kazi yao ya uchunguzi wa shauri hilo. Siku ya kwanza ya mwezi wa kwanza, walikuwa wamekwisha kumaliza uchunguzi wao juu ya wanaume wote waliokuwa wameoa wanawake wa kigeni. Hawa ndio makuhani waliooa wanawake wa kigeni: Wazao wa Yesua, wana wa Yehosadaki na wandugu zake: Maseya, Eliezeri, Yaribu na Gedalia. Hao waliahidi kuwaacha wake zao, na wakatoa kondoo dume kuwa sadaka kwa ajili ya kosa yao. Wazao wa Imeri: Hanani na Zebadia. Wazao wa Harimu: Maseya, Elia, Semaya, Yehieli na Uzia. Wazao wa Pashuri: Eliyoenayi, Maseya, Isimaeli, Netaneli, Yozabadi na Elasa. Kati ya Walawi kulikuwa: Yozabadi, Simei, Kelaya (aliyejulikana pia kwa jina la Kelita), Petahia, Yuda na Eliezeri. Kati ya waimbaji kulikuwa: Eliasibu. Walinzi wa milango: Salumu, Telemu na Uri. Kati ya watu wengine wa Israeli kulikuwa: Wazao wa Parosi: Ramia, Izia, Malkia, Miyamini, Eleazari, Malkia na Benaya. Wazao wa Elamu: Matania, Zakaria, Yehieli Abudi, Yeremoti na Elia. Wazao wa Zatu: Eliyoenayi, Eliasibu, Matania, Yeremoti, Zabadi na Aziza. Wazao wa Bebayi: Yehohanani, Hanania, Zabayi na Atilayi. Wazao wa Bani: Mesulamu, Maluki, Adaya, Yasubu, Seali na Yeremoti. Wazao wa Pahati-Moabu: Adina, Kelali, Benaya, Maseya, Matania, Besaleli, Binui na Manase. Wazao wa Harimu: Eliezeri, Isia, Malkia, Semaya, Simeoni, Benjamina, Maluki na Semaria. Wazao wa Hasumu: Matenayi, Matata, Zabadi, Elifeleti, Yeremayi, Manase na Simei. Wazao wa Bani: Madayi, Amuramu, Ueli, Benaya, Bedeya, Keluhi, Wania, Meremoti, Eliasibu, Matania, Matenayi na Yasu. Wazao wa Binui: Simei, Selemia, Natani, Adaya, Makinadebayi, Sasayi, Sarai, Azareli, Selemia, Semaria, Salumu, Amaria na Yosefu. Wazao wa Nebo: Yeieli, Matitia, Zabadi, Zebina, Yadai, Yoeli na Benaya. Hao wote walioa wanawake wa kigeni na wamoja kati yao walizaa na wanawake wale. Hili ni simulizi la Nehemia mwana wa Hakalia. Ilitukia kwamba, nilipokuwa katika muji mukubwa wa Susani, katika mwezi wa Kisileu wa mwaka wa makumi mbili, Hanani, mumoja wa wandugu zangu, akakuja pamoja na sehemu ya watu toka katika inchi ya Yuda. Nikawauliza juu ya Wayuda wenzetu walioponyoka, ni kusema ambao hawakuhamishiwa Babeli na juu ya Yerusalema. Wao wakaniambia: “Wayuda walioponyoka na kubaki katika jimbo lile, wako katika taabu nao wanazarauliwa. Ukuta wa Yerusalema umebomolewa na milango yake imeteketezwa.” Niliposikia hayo nikaikaa chini na kulia, nikaomboleza kwa siku za kutosha. Nikafunga kula na kumwomba Mungu wa mbinguni, nikisema: “Ee Yawe, Mungu wa mbinguni, wewe ni Mungu unayekuwa mukubwa na wa kutisha, unashika agano lako na kutenda mema kwa wale wanaokupenda na kushika amri zako. Usikilize kwa uangalifu maombi yangu, na uniangalie mimi mutumishi wako, ninapokuomba kwa ajili ya watumishi wako, watu wa Israeli, usiku na muchana. Ninaungama zambi za watu wa Israeli, tulizofanya mbele yako. Mimi pamoja na watu wa jamaa yangu tumefanya zambi. Tumetenda mabaya mbele yako, hatujashika amri zako, masharti na maagizo yako uliyomwagiza mutumishi wako Musa. Kumbuka sasa lile ulilomwambia mutumishi wako Musa, uliposema: ‘Kama hamutakuwa waaminifu, nitawatawanya kati ya mataifa. Lakini mukinirudilia, mukishika amri zangu na kuzifuata hata ingawa nitakuwa nimewatawanya mbali kabisa, nitawarudisha pahali nilipochagua kuwa pahali pangu pa kuabudiwa.’ Watu wa Israeli ni watumishi wako na watu wako uliwakomboa kwa uwezo wako na mukono wako wenye nguvu. Ee Bwana, usikilize maombi yangu mimi mutumishi wako na ya watumishi wako wanaofurahia kukutii wewe. Ninakuomba unifanikishe leo, mimi mutumishi wako, na kunijalia kuhurumiwa na mufalme.” Mimi nilikuwa na madaraka ya kumupa mufalme kinywaji. Katika mwezi wa Nisani, kwa mwaka wa makumi mbili wa utawala wa mufalme Artasasta, wakati divai ilipokuwa mbele yake, nilitwaa divai na kumupatia mufalme. Mpaka sasa nilikuwa sijapata kuwa na huzuni mbele yake. Mufalme Artasasta akaniuliza: “Mbona unaonekana kuwa mwenye huzuni, ingawa hauonekani kuwa mugonjwa? Ninaona una huzuni sana ndani ya moyo wako!” Halafu nikaogopa sana. Nikamujibu: “Ee mufalme, uishi milele! Kwa nini nisikuwe mwenye huzuni wakati Yerusalema ambamo makaburi ya babu zangu uko tupu na milango yake imeteketezwa kwa moto?” Halafu mufalme Artasasta akanijibu: “Sasa unaomba nini?” Nikamwomba Mungu wa mbinguni. Halafu nikamwambia mufalme: “Ee mufalme, ikikupendeza na ikiwa nimepata kukubaliwa mbele yako, ninakuomba unitume katika inchi ya Yuda kusudi niende kuujenga upya muji ambamo muko makaburi ya babu zangu.” Mufalme akaniuliza (malkia akiwa karibu naye): “Utakuwa kule kwa muda gani na utarudi hapa wakati gani?” Ombi langu akalikubali nami nikamujulisha wakati nitakaporudi. Nikamujibu: “Ee mufalme, ikikupendeza, ninaomba nipewe barua kusudi nizipeleke kwa watawala wa jimbo la upande wa magaribi wa muto Furati kusudi waniruhusu nipite mpaka katika inchi ya Yuda. Vilevile ninakuomba kwamba barua ingine iandikwe kwa Asafu mulinzi wa pori la kifalme kusudi anipatie mbao za kutengeneza miimo ya milango ya munara wa hekalu, ukuta wa muji na nyumba yangu nitakamokaa.” Mufalme akakubali ombi langu kwa kuwa Mungu, kwa wema wake, alikuwa pamoja nami. Nilipowafikia wakubwa wa jimbo la upande wa magaribi wa muto Furati, nikawapa barua za mufalme. Mufalme alikuwa amenituma pamoja na wakubwa wa waaskari na waaskari wapanda-farasi. Lakini Sanibalati wa muji wa Muhori na Tobia, Mwamoni, mutumishi wake, waliposikia kwamba nimekuja kwa kushugulikia hali njema ya watu wa Israeli, hawakufurahia kabisa jambo hilo. Hivyo nikafika Yerusalema, nikakaa kule kwa siku tatu. Kisha nikaondoka usiku, mimi pamoja na watu wachache; sikumwambia mutu yeyote yale ambayo Mungu alikuwa ameyaweka ndani ya moyo wangu kwa ajili ya Yerusalema. Lakini siku moja usiku, nikaondoka na kutwaa watu wachache tu. Sikupeleka nyama yeyote isipokuwa punda niliyepanda juu yake mimi mwenyewe. Nikatoka nikipitia kwenye Mulango wa Bonde katika njia inayoelekea kwenye Kisima cha Joka na mulango wa Yalala; nikachunguza kuta za muji wa Yerusalema ambazo zilikuwa zimebomolewa pamoja na milango yake ambayo ilikuwa imeteketezwa kwa moto. Halafu, nikaenda kwenye Mulango wa Chemichemi na kwenye Ziwa la Mufalme. Lakini yule punda niliyepanda juu yake hakuweza kupita. Wakati ule wa usiku, nikapitia katika bonde na kuchunguza ukuta wa muji. Nikarudi nikipitia kwa Mulango wa Bonde. Wakubwa hawakujua pahali nilipokuwa nimekwenda wala nimefanya nini. Tena nilikuwa sijawaambia Wayuda, makuhani, viongozi, wakubwa wala wale watu ambao wangefanya kazi ya kujenga upya muji. Kisha nikawaambia: “Bila shaka munaona magumu yetu kwamba muji wa Yerusalema ni mabomoko na milango yake imeteketezwa kwa moto. Basi, tujenge tena ukuta wa Yerusalema kusudi tusifezeheshwe zaidi.” Nikawaelezea jinsi Mungu alivyokuwa pamoja nami akinitendea kwa wema wake. Nikawaelezea vilevile maneno ambayo mufalme alikuwa ameniambia. Wao waliposikia hayo, wakasema: “Sasa, na tuanze kazi ya ujenzi.” Hivyo wakajitayarisha kwa kazi hiyo njema. Lakini Sanibalati, Muhori, Tobia, Mwamoni mutumishi wake, na Gesemi, Mwarabu, waliposikia hayo, wakatucheka na kutuzomea wakisema: “Ni kitu gani hiki munachotenda? Munataka kumwasi mufalme?” Nikawajibu: “Mungu wa mbinguni atatufanikisha katika kazi hii, nasi tunaokuwa watumishi wake tutaanza kujenga. Lakini ninyi hamuna sehemu au haki wala ukumbusho katika Yerusalema.” Basi Eliasubu, Kuhani Mukubwa, pamoja na wandugu zake waliokuwa makuhani wakasimama na kuanza kujenga Mulango wa kondoo. Wakautakasa na kutia milango yake; wakaitakasa tangia kwenye Munara wa Mia Moja mpaka Munara wa Hananeli. Sehemu iliyofuata ilijengwa upya na watu wa muji wa Yeriko. Nyuma ya hayo aliyefuata ni Zakuri mwana wa Imuri kwa kujenga sehemu ya ukuta. Nao watu wa ukoo wa Hasena wakajenga upya Mulango wa Samaki, wakatia miimo yake, milango, vyuma na vifungio vyake. Sehemu inayofuata ikajengwa upya na Meremoti mwana wa Uria, mujukuu wa Hakosi. Sehemu inayofuata ikajengwa upya na Mesulamu mwana wa Berekia, mujukuu wa Mesezabeli. Sehemu inayofuata ikajengwa upya na Zadoki mwana wa Bana. Sehemu inayofuata ikajengwa na watu kutoka muji wa Tekoa. Lakini viongozi wa muji wakakataa kufanya kazi ya mikono waliyoagizwa kufanya na wasimamizi. Mulango wa zamani; ukajengwa upya na Yoyada mwana wa Pasea, pamoja na Mesulamu mwana wa Besodia, wakatia miimo yake, milango, vyuma na vifungio vyake. Waliowafuata hao katika kazi hiyo ya kujenga upya walikuwa Melatia, Mugibeoni; Yadoni, Mumeronoti pamoja na watu wa muji wa Gibeoni na Misipa waliokuwa chini ya uongozi wa mutawala wa jimbo la upande wa magaribi wa muto Furati. Sehemu inayofuata, ilijengwa upya na Usieli mwana wa Harihaya, mufua zahabu. Sehemu inayofuata mpaka kwenye Ukuta Mupana ikajengwa upya na Hanania, mutengenezaji wa marasi. Sehemu inayofuata ikajengwa upya na Refaya mwana wa Huri, mukubwa wa nusu ya wilaya ya Yerusalema. Sehemu inayofuata, inayoelekeana na nyumba yake ikajengwa upya na Yedaya mwana wa Harumafu. Sehemu inayofuata ikajengwa upya na Hatusi mwana wa Hasabunia. Sehemu inayofuata pamoja na Munara wa Furu vilijengwa upya na Malkiya, mwana wa Harimu akishirikiana na Hasubu mwana wa Pahati-Moabu. Sehemu inayofuata ikajengwa upya na Salumu mwana wa Halohesi, mutawala wa nusu nyingine ya wilaya ya Yerusalema. Alisaidiana na binti zake katika ujenzi huo. Mulango wa Bonde ukajengwa upya na Hanuni pamoja na wakaaji wa muji wa Zanoa. Wakaweka milango pahali pake, wakatia vyuma na vifungio vyake. Wakajenga upya ukuta ukiwa na urefu wa metre mia ine hivi mpaka kwenye mulango wa Yalala. Mulango wa Yalala ukajengwa upya na Malkiya mwana wa Rekabu, mukubwa wa wilaya ya Beti-Hakeremu. Akaweka mulango kwa nafasi yake, akatia vyuma na vifungio vyake. Mulango wa Chemichemi ukajengwa upya na Salumu mwana wa Koli-Hoze, mukubwa wa wilaya ya Misipa. Akaufunika, akauweka mulango kwa nafasi yake, akatia vyuma na vifungio vyake. Kwenye Kisima cha Sela akajenga ukuta unaokuwa karibu na bustani ya kifalme mpaka kwenye ngazi zinazoshuka toka muji wa mufalme Daudi. Sehemu inayofuata mpaka kwenye makaburi ya Daudi, kisima na majengo ya waaskari ikajengwa upya na Nehemia mwana wa Aibuki, mukubwa wa nusu ya wilaya ya Beti-Suri. Nyuma ya hao, Walawi waliendelesha ujenzi mupya wa ukuta. Sehemu inayofuata ikajengwa upya na Rehumu mwana wa Bani, na Hasabia, mutawala wa nusu ya wilaya ya Keila, akajenga upya sehemu ya upande wa wilaya yake. Nyuma yake, sehemu zinazofuata zikajengwa upya na wandugu zao. Sehemu inayofuata ikajengwa upya na Bawayi mwana wa Henadadi, mutawala wa nusu ya wilaya ya Keila. Sehemu inayofuata inayoelekeana na gala ya silaha kwenye pembe ya ukuta ikajengwa upya na Ezeri mwana wa Yesua, mutawala wa Misipa. Sehemu inayofuata tangia kwenye pembe mpaka kwenye mulango wa Eliasibu, Kuhani Mukubwa, ikajengwa upya na Baruku mwana wa Zabayi. Sehemu inayofuata tangia kwenye mulango wa nyumba ya Eliasibu, Kuhani Mukubwa, mpaka mwisho wa nyumba hiyo, ikajengwa upya na Meremoti mwana wa Uria, mujukuu wa Hakosi. Sehemu inayofuata ikajengwa upya na makuhani waliokaa katika sehemu ya mabonde. Benjamina na Hasubu wakajenga upya sehemu inayoelekeana na nyumba yao. Azaria mwana wa Masea, mujukuu wa Anania, akajenga upya sehemu inayoelekeana na nyumba yao. Kuanzia kwenye nyumba ya Azaria mpaka kwenye pembe ya ukuta ikajengwa upya na Binui mwana wa Henadadi. Sehemu inayofuata, tokea kwenye pembe ya ukuta na munara wa nyumba ya kifalme ya juu karibu na kiwanja cha walinzi ikajengwa upya na Palali mwana wa Uzayi. Pedaya mwana wa Parosi, akishirikiana na watumishi wa hekalu waliokaa Ofeli, wakajenga upya sehemu inayoelekeana na Mulango wa Maji, upande wa mashariki na munara murefu. Sehemu ingine inayofuata, ikitokea kwenye munara murefu mpaka kwenye ukuta wa Ofeli ikajengwa upya na wakaaji wa muji wa Tekoa. Juu ya Mulango wa Farasi kulikuwa kundi la makuhani, kila mumoja akajenga sehemu inayoelekeana na nyumba yake. Zadoki mwana wa Imeri akajenga upya sehemu inayoelekeana na nyumba yake. Sehemu inayofuata, ikajengwa upya na Semaya mwana wa Sekania, mulinzi wa Mulango wa Mashariki, Sehemu inayofuata ikiwa ni sehemu yao ya pili ikajengwa upya na Hanania mwana wa Selemia, akishirikiana na Hanuni mwana wa sita wa Zalafi. Mesulamu mwana wa Berekia, akajenga upya sehemu inayoelekeana na chumba chake. Sehemu inayofuata, tokea kwenye nyumba ya watumishi wa hekalu na wachuuzi iliyokuwa inaelekeana na Mulango wa Gereza, karibu na chumba cha juu kwenye pembe upande wa kaskazini-mashariki ikajengwa upya na Malkiya, mufua zahabu. Sehemu ya mwisho kutokea kwa chumba kwenye pembe mpaka kwenye Mulango wa Kondoo ikajengwa upya na wafua zahabu na wachuuzi. Sanibalati aliposikia kwamba tumeanza kazi ya kuujenga upya ukuta akakasirika sana, akaanza kutuchekelea mbele ya warafiki zake na waaskari wa Wasamaria, akisema: “Hawa Wayuda wasiokuwa na nguvu wanafanya nini? Kusudi lao ni kuujenga upya muji? Watatoa sadaka? Wanaweza kumaliza kazi kwa siku moja tu? Wataweza kufanya mawe yaliyolundikana kwenye takataka na yaliyochomwa yakuwe ya kujenga?” Tobia, Mwamoni, aliyekuwa akisimama karibu naye, akatilia mukazo akisema: “Wanajenga nini? Mbweha akipanda juu yake, atabomoa ule ukuta wao wa mawe!” Halafu nikamwomba Mungu nikisema: “Ee Mungu wetu, sikia namna wanavyotuchekelea; urudishe mazarau yao juu yao wenyewe. Uwaache watekwe na kupelekwa katika inchi ya kigeni. Usiwasamehe makosa yao hata kidogo, wala zambi yao usiisamehe hata kidogo; maana wamekukasirikisha mbele ya wajengaji.” Lakini tukaendelea na ujenzi wa ukuta mpaka ukafikia nusu yake kwa sababu watu walikuwa wakitumika kwa bidii. Lakini Sanibalati, Tobia, Waarabu, Waamoni na Waasidodi waliposikia kwamba ujenzi mupya wa ukuta wa Yerusalema ulikuwa unasonga mbele na kwamba nafasi zilizobomoka katika ukuta zimezibwa, wao walizidi kukasirika. Kwa hiyo wakafanya shauri baya kwa kuja pamoja Yerusalema kutushambulia na hivyo kuleta muvurugano katika muji ule. Halafu tukamwomba Mungu wetu na kuweka ulinzi juu yao, muchana na usiku. Watu wa Yuda wakakuwa wanalalamika wakisema: “Tunachoka na kubeba mizigo na bado kuna takataka nyingi za kubeba. Hatuwezi kuendelea kujenga ukuta.” Nao waadui zetu wakakuwa wanasema: “Hawataweza kujua wala kuona, mpaka tutakapokuwa kati yao; tutawaua na kusimamisha kazi.” Wayuda waliokaa kati ya waadui zetu waliposikia maneno yao, mara kwa mara, walitufikia mara kumi wakisema: “Watakuja toka kila pahali wanapokaa na kutushambulia.” Hivyo, kwenye sehemu za chini za ukuta ambazo zilikuwa bado kumalizika, nyuma ya ukuta, katika pahali pa wazi, nikawapanga watu kulingana na jamaa zao wakiwa na mapanga, mikuki na pinde. Nilipoona kwamba watu walikuwa na hofu nikawaambia wakubwa, wasimamizi na watu wote kwa jumla: “Musiwaogope hata kidogo. Mukumbuke Bwana anayekuwa mukubwa na wa kutisha, basi mupigane kwa ajili ya wandugu zenu, wana wenu, wabinti zenu, wake zenu na nyumba zenu.” Waadui waliposikia kwamba tumekwisha kuvumbua mipango yao na kwamba Mungu amevuruga mipango hiyo, ndipo sisi wote tukaurudilia ukuta, kila mumoja akaendelea na kazi yake. Tokea siku ile na kuendelea, nusu ya watumishi wangu wakakuwa wanaendelea na ujenzi wakati nusu ingine ikakuwa inashika ulinzi wakiwa na mikuki, ngao, pinde na nguo za chuma. Viongozi wetu wakakuwa upande wa watu wa Yuda waliokuwa wanajenga ukuta. Hata wale waliokuwa wanabeba vifaa vya ujenzi wakaendelea na kazi mukono mumoja ukiwa na vifaa vya ujenzi na mukono mwingine silaha yake. Kila mujengaji alikuwa na upanga wake ukifungwa kwenye kiuno chake naye akiendelea kujenga. Na mutu wa kupiga baragumu alikuwa karibu nami. Nikawaambia wakubwa, wasimamizi na watu wote kwa jumla: “Kazi ni kubwa, na kuna hatua kubwa kati ya mutu na mwenzake juu ya ukuta. Ukiwa pahali popote unapofanya kazi, mara utakaposikia baragumu, kimbilia kwetu. Mungu wetu atatupigania.” Hivyo, tukaendelea kufanya kazi yetu na nusu ya watu wakishika silaha tangu mapambazuko mpaka nyota zinapoonekana mbinguni. Wakati ule nikawaambia watu: “Kila mwanaume na mutumishi wake atakaa katika Yerusalema usiku, kusudi tukuwe na ulinzi usiku, na wakati wa muchana wataendelea na kazi.” Hivyo ikakuwa mimi, wandugu zangu, watumishi wangu hata na walinzi waliofuatana nami, hatukuvua nguo zetu; kila mumoja wetu akakuwa na silaha yake katika mukono siku zote. Nyuma ya muda kukatokea malalamiko kati ya watu, wanaume na wanawake, wakiwalalamikia wandugu zao Wayuda. Kukatokea waliosema: “Tafazali mutupatie ngano tukule kusudi tuweze kuishi kwa sababu sisi, wana wetu na wabinti zetu tuko wengi.” Na wengine wakalalamika: “Tumeweka rehani mashamba yetu, mizabibu yetu hata na nyumba zetu kwa kupata ngano kwa sababu ya njaa.” Tena kukakuwa hata wale, waliolalamika, wakisema: “Kwa kulipa kodi ya mufalme juu ya mashamba na mizabibu yetu, tulipaswa kukopesha feza. Lakini sisi ni sawa na Wayuda wengine; watoto wetu ni sawa na watoto wao. Hata hivyo, tunawalazimisha watoto wetu kuwa watumwa. Wabinti zetu wamoja wamekwisha kuwa watumwa. Hatuna uwezo wa kuzuia jambo hili maana mashamba yetu na mizabibu yetu inanyanganywa na watu wengine.” Niliposikia malalamiko yao, nikakasirika sana. Nikaamua kukamata hatua. Nikawaonya wakubwa na wasimamizi, nikawaambia: “Munawatesa wandugu zenu.” Nikasema: “Kulingana na uwezo tunaokuwa nao, tumekuwa tukiwanunua tena wandugu zetu Wayuda waliokuwa wameuzishwa kwa watu wa mataifa mengine. Lakini sasa hata munawauzisha wandugu zenu, nasi tunalazimika kuwanunua!” Basi wakanyamaza kimya, bila kuwa na la kujibu. Kisha nikawaambia: “Jambo munalofanya si zuri. Haiwapasi kumwogopa Mungu wetu kwa kuzuia mataifa mengine yanayokuwa waadui zetu yasituzarau? Zaidi ya hayo, mimi mwenyewe, wandugu zangu na watumishi wangu tumewakopesha wandugu zetu feza na ngano. Na hatutadai faida yoyote. Leo hii muwarudishie mashamba yao, mashamba yao ya mizabibu, mashamba ya mizeituni na nyumba zao, hata na faida ya feza, ngano, divai, na mafuta ambayo mulikuwa munawalipisha.” Wao wakaitikia na kusema: “Tutawarudishia na hatutawadai chochote. Tutafanya kama vile ulivyosema.” Nikawaita makuhani mbele, na viongozi wote wakaapa mbele ya makuhani kufanya kama walivyoahidi. Nikakunguta upindo wa kanzu yangu na kusema: “Kila mumoja asiyetimiza ahadi hii Mungu amukungute, amutoe katika nyumba yake na katika kazi yake. Basi, akungutike na kubaki mikono mitupu.” Mukutano muzima wakaitikia, na kusema: “Amina”; wakamusifu Yawe. Watu wakafanya kama vile walivyokuwa wameahidi. Tangu wakati nilipochaguliwa kuwa mutawala wa inchi ya Yuda kwa miaka kumi na miwili ni kusema tangu mwaka wa makumi mbili mpaka mwaka wa makumi tatu na mbili wa utawala kwa mufalme Artasasta, sikukula chakula kinachostahili kukuliwa na mutawala, wala wandugu zangu hawakufanya hivyo. Watawala walionitangulia walikuwa muzigo muzito kwa watu wakiwadai chakula na divai. Zaidi ya hiyo waliwalipisha vikoroti makumi ine vya feza. Hata watumishi wao waliwatesa watu. Lakini, mimi sikufanya hivyo, maana nilimwogopa Mungu. Nilikuwa na juhudi nyingi katika ujenzi mupya wa ukuta huu na sikujipatia hata shamba. Hata watumishi wangu wote walifanya kazi hii kwa bidii. Zaidi ya hayo, kila siku niliwakulisha watu mia moja na makumi tano, kati yao kukiwa Wayuda na wakubwa zaidi ya wale watu waliotufikia toka mataifa jirani. Kila siku, kwa kuwalisha watu hao, nilichinjiwa ngombe dume mumoja na kondoo safi sita na kuku. Kila mara kisha siku kumi nilitoa divai kwa wingi. Lakini zaidi ya haya yote, kwa sababu watu walikuwa na muzigo muzito wa kubeba kila siku, sikutaka posho ya zaidi. Sasa, Ee Mungu wangu, kumbuka wema wangu wote niliowatendea watu hawa. Kisha Sanibalati, Tobia, Gesemi, Mwarabu na waadui zetu wengine, waliposikia kwamba tumemaliza ujenzi wa ukuta na kwamba hakuna pahali penye kubomoka (ingawa tulikuwa bado hatujaweka milango), Sanibalati na Gesemi wakatuma ujumbe kwangu wakisema: “Tukutane kwenye kijiji kimoja katika bonde la Ono.” Lakini walikusudia kunizuru. Basi, nikawatumia wajumbe, nikisema: “Kazi ninayoifanya ni ya lazima sana. Hivyo siwezi kufika kwenu kusudi kazi isipate kusimama.” Wakaendelea kunitumia ujumbe uleule mara ine, lakini nikawapa jibu lilelile. Kwa mara ya tano, Sanibalati akanitumia barua yenye kuwa wazi kwa njia ya mujumbe wake. Na barua yenyewe iliandikwa hivi: Kuna habari zilizoenezwa kati ya mataifa jirani, na Gesemi anahakikisha habari hizi, kwamba wewe pamoja na Wayuda wenzako munakusudia kuasi. Hii ndiyo sababu munaujenga upya ukuta. Kulingana na habari hizo, wewe unakusudia kuwa mufalme wao. Kwa kuhakikisha wazo lako, umejiwekea manabii katika Yerusalema kusudi watangaze kwamba kuna mufalme katika inchi ya Yuda. Maneno haya yataelezwa kwa mufalme Artasasta. Hivyo ninashauri kwamba wewe na mimi tukutane na kuzungumuzia jambo hili. Nami nikamutumia jibu: “Hakuna jambo kama hilo. Habari hizo umezitunga wewe mwenyewe.” Walifanya hivyo kwa kututisha wakifikiri: “Hawataendelea na kazi, kwa hiyo, hakuna litakalotendeka.” Nikamwomba Mungu wangu nikisema: “Lakini sasa, ee Mungu, ninakuomba unipe nguvu.” Nilipokwenda kwa Semaya mwana wa Delaya mujukuu wa Mehetabeli, ambaye hakuruhusiwa kutoka kwake, akaniambia: “Twende tukutane katika nyumba ya Mungu na milango yake tuifunge kwa sababu leo usiku watakuja kukuua.” Lakini mimi nikajiuliza ndani ya moyo: “Mutu kama mimi ataweza kukimbia? Mutu kama mimi anahitaji kuingia katika hekalu apate kuponyesha maisha yake? Sitaingia hata kidogo katika hekalu.” Nikatambua kwamba hakutumwa na Mungu, lakini alikuwa amelipwa na Tobia na Sanibalati atangaze mabaya juu yangu. Alikuwa amelipwa kwa kunitisha kusudi nifanye zambi. Na kwa njia hii wangepata njia ya kuchafua jina langu kwa kunishushia heshima yangu. Nikamwomba Mungu nikisema: “Ee Mungu, kumbuka mambo yote Tobia na Sanibalati waliyotenda, hata yule Noadia, nabii mwanamuke, na manabii wengine waliotaka kuniogopesha.” Basi, ukuta ikamalizika siku ya makumi mbili na tano ya mwezi wa Eluli; nayo ilidumu muda wa siku makumi tano na mbili. Waadui zetu katika mataifa jirani, waliposikia kwamba kazi tumeimaliza, wakaogopa na kupata haya sana; maana walijua hakika kwamba kazi hii ilikamilika kwa musaada wa Mungu wetu. Wakati ule wote, viongozi wa Wayuda walikuwa wakiandikiana na Tobia. Wengi kati ya Wayuda walishirikiana naye kutokana na kiapo chao maana alikuwa mukwe wa Sekania mwana wa Ara. Zaidi ya yote, Yehohanani mwana wake, alikuwa amemwoa binti Mesulamu mwana wa Berekia. Vilevile wakanielezea matendo mema ya Tobia, na wakakuwa wanamupelekea habari zangu. Naye akakuwa ananiandikia barua kwa kunitisha. Nyuma ya ukuta kumalizika, milango yote kuwa tayari, na kuchaguliwa kwa walinzi wa milango, waimbaji na Walawi, nikamuchagua ndugu yangu Hanani kuwa mwangalizi wa Yerusalema akishirikiana na Hanania aliyekuwa jemadari wa waaskari walinzi wa munara katika Yerusalema; kwa sababu alikuwa mutu wa kutegemewa na anayemwogopa sana Mungu, hapakukuwa mwingine aliyelingana naye, nikawaagiza: “Milango isifunguliwe usiku kucha mpaka jua linapokuwa limepanda. Mbele ya kuondoka kwa walinzi ni lazima kufunga milango yote kwa vifungio vyake. Muchague walinzi kati ya wakaaji wa muji wa Yerusalema, kila mumoja akuwe kwa nafasi yake kuelekeana na nyumba yake.” Muji wa Yerusalema ulikuwa mupana na mukubwa, lakini wakaaji wake walikuwa wachache na nyumba zilikuwa hazijajengwa. Mungu akanipa moyo kuwakusanya viongozi na watu kwa kujua ukoo zao. Nikapata kitabu cha ukoo za watu waliorudi toka katika uhamisho mara ya kwanza, na hawa ndio waliokuwa wameandikwa ndani yake. Wale waliokuwa katika uhamisho kule Babeli, walirudi Yerusalema na katika inchi ya Yuda, kila mumoja akarudi katika muji wake. Jamaa zao walikuwa wamekaa Babeli tangu mufalme Nebukadneza alipowahamishia kule wakiwa watumwa. Waliporudi waliongozwa na Zerubabeli, Yesua, Nehemia, Azaria, Ramia, Nahamani, Mordekayi, Bilsani, Misipereti, Bigwayi, Nehumu na Bana. Hii ndiyo jumla ya watu wa ukoo za Waisraeli waliorudi toka katika uhamisho: ukoo wa Parosi: elfu mbili mia moja makumi saba na wawili; ukoo wa Sefatia: mia tatu makumi saba na wawili; ukoo wa Ara: mia sita makumi tano na wawili; ukoo wa Pahati-Moabu, ni kusema wazao wa Yesua na Yoabu: elfu mbili mia nane na kumi na wanane; ukoo wa Elamu: elfu moja mia mbili makumi tano na wane; ukoo wa Zatu: mia nane makumi ine na watano; ukoo wa Zakayi: mia saba na makumi sita; ukoo wa Binui: mia sita makumi ine na wanane; ukoo wa Bebayi: mia sita makumi mbili na wanane; ukoo wa Azgadi: elfu mbili mia tatu makumi mbili na wawili; ukoo wa Adonikamu: mia sita makumi sita na saba; ukoo wa Bigwayi: elfu mbili na makumi sita na saba; ukoo wa Adini: mia sita makumi tano na watano; ukoo wa Ateri (ambao vilevile unaitwa Hezekia): makumi kenda na wanane; ukoo wa Hasumu: mia tatu makumi mbili na wanane; ukoo wa Besayi: mia tatu makumi mbili na wane; ukoo wa Harifu: mia moja kumi na wawili; ukoo wa Gibeoni: makumi kenda na watano. Watu wa miji hii vilevile walirudi: wa muji wa Betelehemu na Netofa: mia moja makumi nane na wanane; wa muji wa Anatoti: mia moja makumi mbili na wanane; wa muji wa Beti-Azimaweti: makumi ine na wawili; wa miji ya Kiriati-Yearimu, Kefira na Beroti: mia saba makumi ine na watatu; wa miji ya Rama na Geba: mia sita makumi mbili na mumoja; wa muji wa Mikimasi: mia moja makumi mbili na wawili; wa miji ya Beteli na Ai: mia moja makumi mbili na watatu; wa muji mwingine wa Nebo: makumi tano na wawili; wa muji mwingine wa Elamu: elfu moja mia mbili makumi tano na wane; wa muji wa Harimu: mia tatu na makumi mbili; wa muji wa Yeriko: mia tatu makumi ine na watano; wa miji ya Lodi, Hadidi na Ono: mia saba makumi mbili na mumoja; wa muji wa Sena: elfu tatu mia tisa na makumi tatu. Hii ndiyo hesabu ya makuhani waliorudi kutoka katika uhamisho: makuhani wa ukoo wa Yedaya, waliokuwa wazao wa Yesua: mia tisa makumi saba na watatu; wa ukoo wa Imeri: elfu moja na makumi tano na wawili; wa ukoo wa Pashuri: elfu moja mia mbili makumi ine na saba; wa ukoo wa Harimu: elfu moja na kumi na saba. Walawi wa ukoo wa Yesua, ni kusema Kadimieli, wazao wa Hodavia waliorudi kutoka katika uhamisho walikuwa makumi saba na wane. Waimbaji: wazao wa Asafu walikuwa mia moja makumi ine na wanane. Walinzi wa milango walikuwa wazao wa: Salumu, Ateri, Talmoni, Akubu, Hatita, Sobayi. Walikuwa mia moja makumi tatu na wanane. Watumishi wote wa hekalu na wazao wa watumishi wa Solomono, waliorudi kutoka katika uhamisho, walikuwa mia tatu makumi tisa na wawili. Watu walirudi kutoka miji hii: Teli-Mela, Teli-Harsa, Kerubu, Adoni, Imeri. Lakini haikuwezekana kuhakikisha kwamba walikuwa wazao wa Waisraeli. Wao walikuwa wazao wa Delaya, Tobia na wa Nekoda, kwa jumla: watu mia sita makumi ine na wawili. Wazao wa ukoo hizi zinazofuata za makuhani vilevile walirudi: ukoo wa Hobaya, wa Hakosi na wa ukoo wa Barzilayi (aliyekuwa ameoa wabinti za Barzilayi, Mugileadi, naye akatwaa jina la ukoo ule.) Hao walitafuta kitabu cha vizazi vyao kati ya wengine walioandikwa katika kitabu cha ukumbusho za ukoo, lakini ukoo wao haukuonekana. Kwa hiyo hawakuruhusiwa kutiwa katika kazi ya ukuhani maana walihesabiwa kuwa wachafu. Mutawala akawaambia kwamba hawaruhusiwi kushiriki kwa chakula kitakatifu sana, mpaka kuhani anayeweza kutumia Urimu na Tumimu afike. Wakubwa wamoja wa ukoo walichangia kazi ya ujenzi. Mutawala wa jimbo alitoa kilo nane za zahabu, mabeseni makumi tano, nguo mia tano na makumi tatu ya makuhani. Wakubwa wa ukoo walitoa kilo mia moja makumi sita na nane za zahabu, na kilo elfu moja mia mbili na makumi tano za feza. Matoleo ya watu wengine wote yalikuwa kilo mia moja makumi sita na nane za zahabu, kilo mia moja makumi ine za feza na nguo za makuhani makumi sita na saba. Basi, makuhani, Walawi, walinzi wa hekalu, waimbaji, pamoja na watu wengine, watumishi wa hekalu na watu wote wa Israeli, wakaishi katika miji yao. Kisha watu wote, kwa nia moja, wakakusanyika katika Yerusalema kwenye kiwanja kinachokuwa karibu na Mulango wa Maji. Wakamwambia Ezra, mwandishi, alete kitabu cha sheria ya Musa ambayo Yawe aliwapa watu wa Israeli. Ezra, ambaye alikuwa kuhani, akaenda na kuleta kitabu cha Sheria ya Musa mbele ya mukutano wote, wanaume na wanawake na yeyote aliyeweza kuelewa ile sheria. Siku hiyo ilikuwa ni siku ya kwanza ya mwezi wa saba. Kisha Ezra akawasomea watu wote wanaume na wanawake na yeyote aliyeweza kuelewa Sheria ya Musa akiwa mbele ya Mulango wa Maji tangu asubui mpaka saa sita za muchana. Watu wote wakatega masikio yao na kusikiliza kwa uangalifu kitabu cha Sheria. Ezra, mwandishi, alikuwa akisimama kwenye mimbari ya mbao iliyotengenezwa kwa kusudi lile; na kwenye mukono wake wa kuume watu hawa walikuwa wakisimama: Matitia, Sema, Anaya, Uria, Hilkia na Masea; na kwenye mukono wake wa kushoto kulikuwa kunasimama watu hawa: Pedaya, Misaeli, Malkiya, Hasumu, Hasubadana, Zakaria na Mesulamu. Ezra akasimama kwenye mimbari mbele ya watu wote, nao wakakuwa wanamukazia macho yao kwa utulivu mukubwa. Mara tu Ezra alipokifungua kitabu cha Sheria, watu wote wakasimama wima. Ezra akamushukuru Yawe, Mungu mukubwa na watu wote wakaitikia: “Amina! Amina!” nao wakiwa wakiinua mikono yao juu. Kisha wakamwabudu Mungu nazo nyuso zao zikigusa chini. Walawi hawa ndio walisaidia kuwaelewesha watu Sheria: Yesua, Bani, Serebia, Yamini, Akubu, Sabetayi, Hodia, Maasea, Kelita, Azaria, Yozabadi, Hanani na Pelaya; na kila mumoja akiwa akisimama pale alipokuwa. Wakasoma vizuri toka kitabu cha Sheria ya Mungu na kuifafanua na watu wote waliweza kuielewa. Watu waliposikia Sheria, wakaguswa ndani ya mioyo yao, halafu wote wakaanza kulia. Hivyo Nehemia aliyekuwa mutawala na Ezra kuhani na mwandishi, pamoja na Walawi waliofundisha watu wakawaambia watu wote: “Siku hii ni siku takatifu kwa Yawe, Mungu wenu, hivyo musiomboleze wala kulia. Sasa murudi kwa nyumba mufanye sherehe, mukule vyakula na kunywa divai nzuri, lakini mukumbuke kuwapelekea wale ambao hawana kitu cha kutosha; maana leo ni siku takatifu kwa Bwana wetu. Musihuzunike kwa sababu furaha Yawe anayowajalia itawapa nguvu.” Halafu, Walawi wakawatuliza watu wote, wakisema: “Munyamaze maana siku ya leo ni takatifu; musihuzunike.” Watu wote wakarudi kwao kwa kula na kunywa, wakifurahi na kuwagawanyia wengine chakula kwa sababu walielewa yote waliyotangaziwa. Kesho yake, wakubwa wa ukoo pamoja na makuhani na Walawi wakakusanyika kwa Ezra mwandishi, kwa kujifunza Sheria. Wakagundua kwamba, imeandikwa katika kitabu cha Sheria kuwa Yawe alimwamuru Musa, kwamba watu wanapaswa kukaa katika vibanda wakati wa sikukuu ya mwezi wa saba. Hivyo wakatangaza katika miji yao yote na kule Yerusalema, wakisema: “Mwende kwenye milima, mulete matawi ya mizeituni, mizeituni ya pori, mihadasi, mingazi na miti mingine kwa kujenga vibanda, kama vile ilivyoandikwa.” Basi, watu wakaenda kuleta matawi, wakajenga vibanda kila mutu kwenye dari na kwenye baraza ya nyumba yake, kwenye baraza za nyumba ya Mungu, kwenye uwanja wa kiwanja cha Mulango wa Maji na kiwanja cha Mulango wa Efuraimu. Watu wote waliorudi kutoka katika uhamisho wakatengeneza vibanda wakaishi ndani yake. Hii ilikuwa ni mara ya kwanza watu kuishi katika vibanda tangu wakati Yesua mwana wa Nuni alipokuwa akiishi. Watu wakafurahi sana. Kila siku, tangu siku ya kwanza mpaka ya mwisho, Ezra aliwasomea watu kitabu cha Sheria ya Mungu. Wakafanya sikukuu ile kwa muda wa siku saba. Na siku ya nane wakafanya mukutano mukubwa wa kufunga sikukuu, kama vile ilivyoagizwa. Siku ya makumi mbili na ine ya mwezi ule wa saba, watu wa Israeli wakakusanyika, wakifunga kula na kuvaa nguo za magunia na kujipakaa udongo juu ya kichwa kwa kuonyesha majuto juu ya zambi zao. Wakati ule, walikuwa wamejitenga mbali na watu wa mataifa mengine, wakasimama na kuungama zambi zao na maovu ya babu zao. Kwa muda wa yapata saa tatu, walisimama wakati Sheria ya Yawe, Mungu wao, ikisomwa. Na kwa saa tatu zilizofuata, walikuwa wakitubu na kumwabudu Yawe, Mungu wao. Kuliwekwa daraja la Walawi; pale kulisimama Yesua, Bani, Kadimieli, Sebania, Buni, Serebia, Bani na Kenani. Wakamwomba kwa sauti kubwa Yawe, Mungu wao. Walawi, ni kusema Yesua, Kadimieli, Bani, Hasabuea, Serebia, Hodia, Sebania na Petahia, wakawaambia watu: Musimame na kumusifu Yawe, Mungu wenu. Mumusifu milele na milele! Na watu wakasifu jina lako tukufu, ambalo linatukuka kuliko baraka na sifa zote. Ezra akaomba akisema: Wewe peke yako ndiwe Yawe! Ulifanya mbingu na jeshi lake lote, dunia na vyote vinavyokuwa ndani yake, bahari na vyote vinavyokuwa ndani yake. Unavipatia uzima, na jeshi lote la mbinguni linakuabudu wewe. Wewe ndiwe Yawe, Mungu uliyemuchagua Abramu. Ukamutoa toka Uri ya Wakaldea na kumupa jina la Abrahamu. Ukamwona kuwa wa haki mbele yako; ukafanya agano naye kuwapa wazao wake inchi ya Wakanana, Wahiti, Waamori, Waperizi, Wayebusi na Wagirgasi. Na ahadi yako ukaitimiza; maana wewe ni mwaminifu. Uliyaona mateso ya babu zetu walipokuwa katika inchi ya Misri, na walipokuomba musaada kwenye bahari Nyekundu ukawasikiliza. Ulifanya miujiza na maajabu mbele ya Mufalme wa Misri, watumishi wake wote na watu wote wa inchi yake; maana ulijua kwamba waliwagandamiza babu zetu. Ukajipatia utukufu unaokuwa mpaka leo. Uligawanya bahari katikati mbele yao, nao wakapita katikati ya bahari, pahali pakavu. Lakini ukawatupa Wamisri waliowafuatilia kama jiwe zito ndani ya maji mengi. Muchana uliwaongoza kwa nguzo la wingu, na usiku uliwaongoza kwa nguzo la moto kwa kuwaangazia njia ya kufuata. Kule kwa mulima Sinai ulishuka toka mbinguni na kuzungumuza nao. Ukawapa maagizo safi, sheria za kweli, masharti mazuri na amri. Kwa njia ya Musa, mutumishi wako, ukawajulisha siku zako za Sabato takatifu na ukawaagiza kuzifuata amri, masharti na sheria ulizowaamuru. Walipokuwa na njaa, ukawapa chakula kutoka mbinguni. Walipokuwa na kiu, ukawapa maji kutoka katika jiwe. Ukawaagiza kurizi inchi uliyokuwa umewaahidi. Lakini wao na babu zetu wakakuwa na kiburi na wakakuwa wagumu wakakataa kufuata maagizo yako. Wakakataa kutii; hawakukumbuka maajabu uliyofanya kati yao. Wakakuwa wagumu, wakajichagulia kiongozi wa kuwarudisha katika utumwa katika inchi ya Misri. Lakini wewe Mungu uko mwepesi kwa kusamehe, mwenye huruma na rehema, haukasiriki upesi, uko mwema sana. Haukuwatupilia hata walipojitengenezea sanamu ya mwana-ngombe na kusema: “Huyu ndiye Mungu wetu aliyetutoa kutoka katika inchi ya Misri.” Wakakuchukiza sana lakini wewe kwa rehema zako nyingi haukuwatupilia kule katika jangwa. Nguzo la wingu lililowaongoza muchana, wala nguzo la moto lililowaangazia katika njia usiku, havikuondoka. Ukawapa Roho wako mwema kuwashauria; ukawapa mana kuwa chakula chao, na maji ya kunywa kwa kutuliza kiu chao. Ukawatunza katika jangwa kwa miaka makumi ine na hawakukosa kitu chochote; nguo zao hazikuchakaa wala miguu yao haikuvimba. Ukawapatia ushindi juu ya falme na mataifa, ukawafanyia mengi kila upande. Wakashinda inchi ya Hesiboni iliyotawaliwa na mufalme Sihoni; na tena wakashinda inchi ya Basani iliyotawaliwa na mufalme Ogi. Ukafanya wazao wao kuwa wengi kama nyota za mbinguni; ukawaleta katika inchi uliyowaahidi babu zao. Hivyo, hao wazao wakakuja na kurizi inchi. Ulishinda Wakanana na kuwatia katika mikono yao. Watu wako waliweza kuwatendea vile walivyotaka wafalme na watu wa inchi hiyo. Wakateka miji yenye kuta, wakatwaa inchi yenye utajiri, nyumba zenye vitu vingi vizuri, visima vilivyochimbwa, mashamba ya mizabibu na mizeituni pamoja na miti yenye matunda kwa wingi. Hivyo wakakula, wakashiba na kunenepa na kufurahia wema wako. Lakini hawakukuwa waaminifu kwako. Wakakuasi, wakaacha sheria yako na kuwaua manabii waliowaonya kusudi wakurudilie wewe. Wakatenda zambi kubwa mbele yako. Hivyo, ukawatia katika mikono ya waadui zao, nao wakawatesa. Lakini wakiwa katika mateso yao, wakakulilia, nawe ukawasikiliza kutoka mbinguni. Na kwa rehema zako nyingi, ukawatumia viongozi wa kuwaokoa; nao wakawakomboa toka katika mikono yao. Lakini amani ilipopatikana wakatenda zambi tena mbele yako, nawe ukawaacha watiwe katika mikono ya waadui zao wawatawale. Hata hivyo, walipotubu na kukulilia ukawasikiliza kutoka mbinguni. Na kwa kulingana na rehema zako nyingi, ukawaokoa mara nyingi. Ukawaonya kusudi warudilie Sheria yako, hata hivyo, kwa kiburi chao, wakaacha kutii amri zako. Wakaasi maagizo yako, ambayo kwa njia yake mutu akiyatii, ataishi. Wakakuwa wenye kiburi vilevile wakakuwa wagumu, na wakakataa kuwa watiifu. Ukawavumilia kwa miaka mingi, na kuwaonya kwa njia ya roho wako kwa kupitia manabii wako; hata hivyo hawakusikiliza. Basi ukawaacha ukawatia katika mikono ya mataifa mengine. Hata hivyo, kutokana na rehema zako nyingi, haukuwaachilia waangamie kabisa au kuwatupilia, maana wewe ni Mungu mwenye huruma na rehema. Kwa hiyo, ee Mungu wetu, Mungu mukubwa, mwenye nguvu na wa kutisha, wewe unashika agano lako na kutenda wema. Mateso yaliyotupata, sisi, wafalme wetu, wakubwa wetu, makuhani wetu, manabii wetu, babu zetu na watu wako wote tangu wakati wa wafalme wa Asuria mpaka leo, usiyaone kuwa ni madogo. Hata hivyo, una haki kwa kutuazibu hivyo; maana wewe umekuwa mwaminifu wakati sisi tumekuwa watenda maovu. Wafalme wetu, wakubwa wetu, makuhani wetu na babu zetu hawakushika Sheria yako wala kujali amri zako na maonyo yako uliyowapa. Hawakukutumikia katika ufalme wao, wala walipofurahia mema yako mengi uliyowajalia kwa wingi, katika inchi kubwa na yenye mboleo uliyowapa hawakuyaacha matendo yao maovu. Na leo tumekuwa watumwa; tuko watumwa katika inchi uliyowapa babu zetu kwa kufurahia matunda yake na mazao yake mema. Kwa sababu ya zambi zetu, utajiri wa inchi hii unawaendea wafalme uliowaleta kwa kututawala. Wanatutawala jinsi wanavyopenda hata na nyama wetu wa ufugo wanawatendea jinsi wanavyopenda, tuko katika taabu kubwa sana. Kutokana na haya yote yaliyotokea, sisi tunaweka agano imara kwa maandiko na wakubwa wetu, Walawi na makuhani wanatia sahihi zao na muhuri wao. Sisi wote, watu wa Israeli, makuhani, Walawi, walinzi wa milango, waimbaji, watumishi wa hekalu na watu wote waliojitenga na mataifa jirani kufuata sheria ya Mungu pamoja na wake zao, wana wao, na wabinti zao, wote wenye maarifa na ufahamu, tunaungana na wandugu zetu, wakubwa wetu, katika kufanya kiapo na kwamba tukivunja kiapo hiki tutapata azabu, na tunaapa kwamba tutaishi kwa kufuata sheria ya Mungu ambayo alitoa kwa njia ya Musa, mutumishi wake; tena tutatii yote ambayo Yawe, Mungu wetu, anatuamuru; na kwamba tutashika maagizo na masharti yake. Wabinti zetu hatutawaoesha kwa watu wa inchi hii na wala wana wetu hawataoa kwao. Ikiwa watu hao wanaleta biashara au ngano kwa kuuzisha siku ya Sabato, sisi hatutanunua siku hiyo wala siku nyingine yoyote inayokuwa takatifu. Mwaka wa saba hatutalima mashamba na madeni yote tutayafuta. Tunajiwekea sheria juu yetu kwamba, kwa mwaka tutatoa sehemu moja ya tatu ya kikoroti kimoja cha feza kwa ajili ya kazi za nyumba ya Mungu: kwa ajili ya mikate mitakatifu, sadaka za unga za kawaida, sadaka za kuteketezwa kwa moto za kawaida, sadaka za siku za Sabato, sikukuu za mwandamo wa mwezi, sikukuu nyingine zilizowekwa, vitu vingine vitakatifu, sadaka za kusamehewa zambi, kwa kuwafanyia upatanisho watu wa Israeli na kazi nyingine zozote za nyumba ya Mungu wetu. Sisi wote, watu wote, makuhani na Walawi tutapiga kura kila mwaka kwa kuchagua ukoo utakaoleta kuni za kuteketeza sadaka juu ya mazabahu ya Yawe, Mungu wetu, kufuatana na Sheria. Tunaahidi kuleta kila mwaka malimbuko yetu ya mazao na ya matunda ya kila muti kwenye nyumba ya Yawe. Kwa kufuata vile ilivyoandikwa katika Sheria kila muzaliwa wa kwanza wa kiume kati ya wana wetu, katika nyumba zetu, atapelekwa katika nyumba ya Mungu wetu kwa makuhani wanaotumika mule, vilevile tutapeleka kila muzaliwa wa kwanza dume wa ngombe zetu, mbuzi zetu na kondoo zetu. Kila unga wetu wa kwanza, matoleo yetu, matunda ya miti, divai na mafuta tutavileta kwa kuhani kwenye vyumba vya nyumba ya Mungu wetu. Tena tutaleta zaka zetu za mazao yetu kwa Walawi, maana ndio wanaoshugulika na kukusanya zaka zile katika vijiji vyetu. Kuhani, wa uzao wa Haruni atakuwa pamoja na Walawi wanapokea zaka. Halafu Walawi watapeleka sehemu moja ya kumi ya zaka zote zilizotolewa katika nyumba ya Mungu kwenye vyumba na gala. Watu wa Israeli na Walawi watayapeleka matoleo ya ngano, divai na mafuta ya zeituni kwenye vyumba ambamo vyombo vya Pahali Patakatifu vinapochungwa na ambamo makuhani, walinzi wa milango na waimbaji wana vyumba vyao. Na siku zote tutashugulikia nyumba ya Mungu wetu. Kisha, viongozi wa watu wakakaa katika Yerusalema; watu wengine wote, wakapiga kura kati ya kila jamaa kumi kwa kuchagua jamaa moja itakayokaa katika Yerusalema, muji mutakatifu. Jamaa zingine tisa zikakaa katika miji yao mingine. Watu wakawasifu wale wote waliokubali kukaa katika Yerusalema. Na katika miji mingine, watu wa Israeli, makuhani, Walawi, walinzi wa milango na wazao wa watumishi wa Solomono, walikaa katika maeneo yao wenyewe, katika miji yao. Watu wamoja wa kabila la Yuda na wa kabila la Benjamina walikaa katika Yerusalema: Hawa ndio watu wa ukoo wa Yuda waliokaa Yerusalema: Ataya mwana wa Uzia, mujukuu wa Zakaria mwana wa Amaria mwana wa Sefatia mwana wa Mahalaleli wa uzao wa Peresi; Maseya mwana wa Baruku mwana wa Koli-Hoze mwana wa Hazaya mwana wa Adaya mwana wa Yoyaribu mwana wa Zekaria, Mushilo. Wazao wote wa Peresi waliokaa katika Yerusalema walikuwa wanaume mashujaa mia ine makumi sita na wanane. Watu wa ukoo wa Benjamina waliokaa katika Yerusalema ni: Salu, mwana wa Mesulamu mwana wa Yoedi mwana wa Pedaya mwana wa Kolaya mwana wa Maseya mwana wa Itieli na mwana wa Yesaya. Nyuma ya huyo kulikuwa Gabayi na Salayi. Jumla yao mia tisa makumi mbili na wanane. Yoeli mwana wa Sikiri, alikuwa ndiye mukubwa wao; naye Yuda mwana wa Hasenua alikuwa mukubwa wa pili wa muji. Makuhani waliokaa katika Yerusalema walikuwa: Yedaya mwana wa Yoyaribu, Yakini, Seraya mwana wa Hilkia mwana wa Mesulamu mwana wa Zadoki mwana wa Merayoti mwana wa Ahitubu aliyekuwa musimamizi wa nyumba ya Mungu, pamoja na wandugu zao waliofanya kazi katika hekalu walikuwa mia nane makumi mbili na wawili. Pamoja na hao, kulikuwa Adaya mwana wa Yerohamu, mwana wa Pelalia mwana wa Amsi mwana wa Zakaria mwana wa Pasuri mwana wa Malkiya; vilevile wandugu zake waliokuwa wakubwa wa jamaa za baba zao; wote pamoja walikuwa watu mia mbili makumi ine na wawili. Vilevile kulikuwa Amasayi, mwana wa Azareli mwana wa Azayi mwana wa Mesilemoti mwana wa Imeri, pamoja na wandugu zao; wote wakiwa mia moja makumi mbili na wanane, watu mashujaa. Na mukubwa wao alikuwa Zabdieli mwana wa Hagedolimu. Nao Walawi waliokaa katika Yerusalema walikuwa: Semaya mwana wa Hasubu mwana wa Azirikamu mwana wa Hasabia, na mwana wa Buni. Sabetayi na Yozabadi, wakubwa wa ukoo wa Walawi, walikuwa wasimamizi wa kazi za inje ya nyumba ya Mungu, na Matania mwana wa Mika mwana wa Zabudi, wa uzao wa Asafu, aliyekuwa kiongozi wakati wa kuomba maombi ya shukrani. Bakubukia alikuwa musaidizi wake. Pamoja nao kulikuwa Abuda mwana wa Samua mwana wa Galali wa uzao wa Yedutuni. Walawi wote waliokaa katika Yerusalema, muji mutakatifu, walikuwa mia mbili makumi munane na wane. Walinzi wa milango waliokaa katika Yerusalema walikuwa: Akubu na Talmoni pamoja na wandugu zao waliokuwa wakilinda milango, walikuwa mia moja makumi saba na wawili. Watu wengine wa Israeli, makuhani na Walawi walikaa katika miji ya Yuda, kila mumoja katika urizi wake. Lakini watumishi wa hekalu walikaa Yerusalema katika eneo la Ofeli wakiwa chini ya usimamizi wa Ziha na Gisipa. Kiongozi wa Walawi waliokaa Yerusalema alikuwa, Uzi, mwana wa Bani mwana wa Hasabia mwana wa Matania mwana wa Mika wa ukoo wa Asafu, waliokuwa waimbaji, viongozi waangalizi wa shuguli za nyumba ya Mungu. Mufalme alikuwa ametoa amri juu ya utaratibu wa kazi zao na mahitaji yao ya kila siku. Petahia mwana wa Mesezabeli, wa ukoo wa Zera katika kabila la Yuda, alikuwa musimamizi wa mufalme juu ya mambo yote ya watu wa Yuda. Watu wengine walikaa katika miji karibu na mashamba yao. Watu wamoja wa kabila la Yuda walikaa Kiriati-Arba, Diboni na Yekabuseli pamoja na vijiji vilivyoizunguka. Wengine vilevile walikaa katika miji ya Yesua, Molada, Beti-Peleti, Hazari-Suali na Beri-Seba pamoja na vijiji vilivyoizunguka. Wengine walikaa katika muji wa Ziklagi, Mekona na vijiji vilivyoizunguka. Wengine walikaa katika miji ya Eni-Rimoni, Sora, Yarmuti; Zanoa na Adulamu pamoja na vijiji vilivyoizunguka, Lakisi na mashamba yanayouzunguka, na katika Azeka pamoja na vijiji vinavyouzunguka. Hii ina maana kwamba watu wa Yuda walikaa katika eneo linalokuwa kati ya Beri-Seba upande wa kusini na Bonde la Hinomu upande wa Kaskazini. Watu wa kabila la Benjamina walikaa Geba, Mikimasi, Ai, Beteli na vijiji vinavyoizunguka. Wengine walikaa Anatoti, Nobu, Anania, Hazori, Rama, Gitaimu, Hadidi, Seboimu, Nebalati, Lodi na Ono lililokuwa Bonde la Wafundi. Walawi wamoja wa Yuda wakachanganyika na watu wa Benjamina. Walawi walikuwa: Yesua, Binui, Kadimieli, Serebia, Yuda na Matania, ambaye alishugulika na usimamizi wa nyimbo za shukrani akishirikiana na ndugu zake. Nao Bakubukia na Uno warafiki zao, walisimama wakielekeana nao katika ibada. Wakati wa Eliasibu, Yoyada, Yohanani na Yadua wakubwa wa jamaa za Walawi waliandikwa; vilevile wakati wa utawala wa mufalme Dario wakubwa wa jamaa za makuhani waliandikwa. Wakubwa wa jamaa za ukoo wa Lawi walioandikwa katika kitabu cha Mambo ya Siku mpaka wakati wa Yohanani mujukuu wa Eliasibu. Viongozi wa Walawi Hasabia, Serebia, Yesua mwana wa Kadimieli walisimama kuelekeana na wandugu zao walipangwa kwa kuimba nyimbo za kusifu na kushukuru, kufuatana na amri ya mufalme Daudi, mutu wa Mungu. Walinzi wa milango walikuwa: Matania, Bakubukia, Obadia, Mesulamu, Talmoni na Akubu; vilevile hao walikuwa walinzi wa gala. Watu hao waliishi wakati wa Yoyakimu mwana wa Yesua mujukuu wa Yosadaki na vilevile wakati wa Nehemia aliyekuwa liwali wa jimbo; na hata wakati wa Ezra kuhani na mwandishi. Kisha wakati wa kuzindua ukuta wa Yerusalema Walawi wakatafutwa kila pahali walipokaa kwa kuja Yerusalema kusherehekea kwa furaha pamoja na shukrani na nyimbo, wakitumia matoazi, vinubi na zeze. Wazao wa waimbaji wakakusanyika kutoka vijiji vya Yerusalema na vijiji vya Wanetofati, vilevile kutoka Beti-Gilgali, eneo la Geba na Azimaweti, kwa sababu waimbaji walikuwa wamejijengea vijiji kandokando ya Yerusalema. Makuhani na Walawi wakajitakasa, vilevile wakatakasa watu, milango na ukuta. Nikawakusanya viongozi wote wa Yuda kwenye ukuta na kutenga waimbaji katika makundi mawili makubwa yaliyoimba nyimbo za shukrani wakiwa katika maandamano. Kundi moja lilielekea upande wa kuume wa ukuta mpaka kwenye Mulango wa Takataka. Waimbaji hao walifuatwa na Hosaya akiwa pamoja na nusu ya viongozi wa Yuda. Pamoja naye walikwenda Azaria, Ezra, Mesulamu, Yuda, Benjamina, Semaya na Yeremia. Wazao hawa wa makuhani walikuwa na baragumu: Zakaria, mwana wa Yonatani mujukuu wa Semaya aliyekuwa mwana wa Matania mwana wa Mikaya mwana wa Zakuri mwana wa Asafu. Ndugu zake hawa waliimba kwa ala za muziki za mufalme Daudi, mutu wa Mungu, ni kusema Semaya, Azareli, Milalayi, Gilalayi, Maayi, Netaneli, Yuda na Hanani, wakatanguliwa na Ezra mwandishi. Kwenye Mulango wa Chemichemi walipanda ngazi kuelekea muji wa Daudi, wakapita nyumba ya kifalme ya Daudi, na kuelekea nyuma kwenye ukuta mpaka kwenye Mulango wa Maji, upande wa mashariki wa muji. Kundi lingine lililoimba nyimbo za shukrani lilielekea upande wa kushoto juu ya ukuta. Mimi nikafuatana na kundi hili pamoja na nusu ya watu. Tukapitia kwenye Munara wa Furu mpaka kwenye Ukuta Mupana. Na kutoka pale, tukapitia kwenye Mulango wa Efuraimu, Mulango wa Yesana, Mulango wa Samaki, Munara wa Hananeli, Munara wa Mia moja mpaka kwenye Mulango wa Kondoo. Tulimalizia maandamano yetu kwenye Mulango wa Walinzi. Hivyo, makundi yote mawili yaliyokuwa yanaimba nyimbo za shukrani yakasimama katika nyumba ya Mungu, pamoja nami na nusu ya viongozi; hata na makuhani waliokuwa na baragumu: Eliakimu, Maseya, Miniamini, Mikaya, Eliyoenayi, Zakaria na Hanania. Hao walifuatwa na Maseya, Semaya, Eleazari, Uzi, Yehohanani, Malkiya, Elamu na Ezeri. Waimbaji waliimba wakiongozwa na Yesirahia. Siku hiyo, watu wakatoa sadaka nyingi na kufurahi maana Mungu aliwafanya kuwa na furaha kubwa. Vilevile wanawake na watoto, wote wakafurahi. Vigelegele vya furaha toka katika Yerusalema vikasikilika mbali. Wakati ule wakachagua watu wa kuchunga vyumba vya gala ambamo matoleo kwa ajili ya hekalu yaliwekwa, malimbuko ya kwanza, zaka na kuyakusanya kutoka katika mashamba ya miji, kwa ajili ya makuhani na Walawi kama ilivyotakiwa na Sheria. Watu wote wakafurahia makuhani na Walawi waliotumika, kwa sababu walifanya ibada ya Mungu wao na ibada ya utakaso, kama vile waimbaji walivyoimba hata walinzi wa milango kulingana na agizo la mufalme Daudi na mwana wake Solomono. Tangu wakati wa mufalme Daudi na Asafu kulikuwa kiongozi wa waimbaji, na kulikuwa nyimbo za sifa na shukrani kwa Mungu. Watu wote wa Israeli, tangu wakati wa Zerubabeli na Nehemia, walitoa matoleo ya kila siku kwa ajili ya waimbaji na walinzi wa milango. Zaidi ya yote, watu wa Israeli wakatoa matoleo kwa ajili ya Walawi, nao Walawi wakatenga sehemu kwa ajili ya wazao wa Haruni. Katika siku ile ya sherehe, kitabu cha Musa kikasomwa na ikajulikana kwamba Waamoni na Wamoabu hawaruhusiwi kuingia katika mukutano wa watu wa Mungu. Kwa sababu watu wa Israeli, walipokuwa wanasafiri toka Misri, wao hawakuwapa chakula wala maji ya kunywa, pahali pake wakamulipa Balamu kwa kuwalaani watu wa Israeli, lakini Mungu wetu akageuza laana yao kuwa baraka. Watu wa Israeli waliposikia Sheria hiyo wakawatenga watu wa mataifa mengine. Mbele ya siku ya sherehe, kuhani Eliasibu aliyekuwa amechaguliwa kwa kulinda vyumba vya nyumba ya Mungu wetu, na mwenye ushirika mwema na Tobia, alimuruhusu Tobia kutumia chumba kikubwa ambamo pale mbele walikuwa wakiweka sadaka za unga, ubani, vyombo, zaka za unga, divai, mafuta; vitu hivyo vyote Waisraeli walivyoagizwa kutoa kwa Walawi, waimbaji, walinzi wa milango, na matoleo kwa makuhani. Wakati mambo haya yalipokuwa yanatendeka mimi sikukuwa Yerusalema; maana katika mwaka wa makumi tatu na mbili wa utawala wa mufalme Artasasta wa Babeli, nilikuwa nimeomba ruhusa; nami nikaenda kwake. Niliporudi Yerusalema ndipo nikagundua uovu wa Eliasibu wa kumutayarishia Tobia chumba katika kiwanja cha nyumba ya Mungu. Nikakasirika sana na nikavitupilia inje vyombo vyote vya Tobia. Nikaamuru watu, nao wakatakasa vyombo hivyo halafu nikarudisha mule vifaa vya nyumba ya Mungu, pamoja na sadaka ya unga na ubani. Tena nikagundua kwamba Walawi hawakupewa haki zao; na matokeo yake ni kwamba Walawi na waimbaji waliokuwa wakifanya kazi pale mbele, sasa walikwisha kurudilia mashamba yao. Nikawakaripia viongozi, nikisema: “Kwa nini nyumba ya Mungu imeachwa?” Nikawakusanya pamoja na kuwarudisha katika kazi. Kisha, watu wote wa Israeli, wakaanza tena kuleta zaka zao za unga, divai na mafuta kwenye gala. Nikachagua watu hawa kuwa walinzi wa gala: kuhani Selemia, Zadoki mwandishi na Pedaya, Mulawi. Hanani mwana wa Zakuri mujukuu wa Matania akakuwa musaidizi wao. Walikuwa waaminifu na kazi yao ilikuwa kuwagawanyia wandugu zao mahitaji yao. Ee Mungu wangu, unikumbuke kwa ajili ya haya yote na usiyasahau matendo yangu mema niliyofanya kwa ajili ya nyumba yako na kwa ajili ya kazi yako. Wakati uleule, nikawaona watu wa Yuda wakikamua zabibu katika vikamulio siku za Sabato. Tena wengine walikuwa wakiwabebesha punda wao ngano, divai, zabibu, tini na vitu vingine wakivipeleka Yerusalema. Nikawaonya kwamba hawana ruhusa ya kuuzisha katika siku hiyo. Watu wengine toka muji wa Tiro walileta samaki na biashara nyingine Yerusalema na kuwauzishia watu wetu siku ya Sabato. Nikawakaripia viongozi wa watu wa Yuda, nikisema: “Uovu gani huu munaofanya, kuichafua siku ya Sabato? Babu zetu hawakufanya uovu wa namna hiihii na kumusukuma Mungu wetu kutuletea hasara pamoja na muji huu? Na munazidi kuamusha kasirani yake juu ya watu wa Israeli kwa kuchafua siku ya Sabato.” Halafu, nikaamuru kwamba milango ya Yerusalema ifungwe wakati siku ya Sabato inapoanza magaribi, wakati giza linapoanza kuingia, na isifunguliwe mpaka Sabato imekwisha. Nikaweka watumishi wangu wamoja kwenye milango na kuwaagiza kwamba kitu chochote kisiletwe katika muji siku ya Sabato. Mara mbili au tatu hivi wachuuzi waliokuwa wakiuzisha biashara ya aina mbalimbali walipaswa kulala inje ya muji. Nikawaonya na kuwaambia: “Hakuna maana kulala inje ya muji. Mukijaribu tena nitatumia nguvu.” Hivyo tangu wakati ule hawakurudi tena siku ya Sabato. Nikaagiza Walawi kujitakasa na kwenda kulinda milango kwa kutakasa siku ya Sabato. Ee, Mungu wangu, unikumbuke hata na kwa hili vilevile unihurumie kutokana na rehema zako kubwa. Tena wakati ule nikaona Wayuda waliooa wanawake toka Asidodi, Amoni na Moabu; na nusu ya watoto wao waliosema luga ya Kiasidodi au luga nyingine na hawakuweza kusema luga ya inchi ya Yuda. Nikawakaripia na kuwalaani, hata nikawapiga wamoja kati yao na kuwaongoa nywele zao. Nikawalazimisha kuapa kwa jina la Mungu, nikisema: “Wabinti zenu musiwaoeshe kwa vijana wao, wala wabinti zao wasiolewe na vijana wenu au na ninyi wenyewe. Si Solomono alitenda zambi kwa sababu ya wanawake wa namna hiyo? Yeye alikuwa mufalme mukubwa kuliko wafalme wa mataifa mengine. Mungu akamupenda na akamufanya kuwa mufalme juu ya watu wote wa Israeli, hata hivyo wanawake wa mataifa mengine, wakamusukuma kutenda zambi. Basi, sasa tufuate mufano wenu na tutende zambi hii kubwa ya kutomutii Mungu wetu kwa kuoa wanawake wa kigeni?” Mumoja kati ya wana wa Yoyada mwana wa Kuhani Mukubwa Eliasibu, alioa binti wa Sanibalati kutoka muji wa Beti-Horoni, kwa sababu hiyo nikamufukuza kutoka mbele yangu. Ee Mungu, kumbuka jinsi watu walivyochafua ukuhani na agano la kikuhani na la Walawi. Nikawatakasa watu kutokana na chochote kilichokuwa cha kigeni. Nikatayarisha utaratibu kwa ajili ya makuhani na Walawi juu ya kazi ya kila mumoja wao. Nikaagiza matoleo ya kuni kufanyika katika wakati unaopaswa na malimbuko wakati wake. Ee Mungu wangu, unikumbuke kwa ajili ya haya yote na unijalie mema. Mufalme Ahasuero alipotawala ufalme wake ulikuwa na majimbo mia moja makumi mbili na saba, toka Uhindi mpaka Etiopia. Kiti chake cha kifalme kilikuwa katika muji mukubwa Susani. Katika mwaka wa tatu wa utawala wake, mufalme Ahasuero akaandaa karamu kwa ajili ya viongozi na watumishi wake wa serikali, wakubwa wa majeshi ya Persia na Media, watu wenye heshima na wakubwa wa majimbo. Basi, kwa muda wa miezi sita, Ahasuero akaonyesha utajiri wa ufalme wake mutukufu, na sifa ya utawala wake. Muda ule ulipomalizika, mufalme aliandaa karamu kwa ajili ya watu wote wa muji mukubwa wa Susani, wakubwa kwa wadogo. Karamu hiyo iliyokamata muda wa siku saba, ilifanyika ndani ya kiwanja, katika bustani ya nyumba ya kifalme. Pahali pale kulikuwa kumepambwa kwa mapazia ya pamba ya rangi nyeupe na vitambaa vya rangi ya samawi. Mapazia hayo yalikuwa yamefungiwa pete za feza kwa kamba za kitani safi nyekundu-nyeusi, na kutundikwa kwenye nguzo za mawe ya marimari. Viti vya zahabu na feza vilikuwa vimewekwa kwenye sakafu iliyotengenezwa kwa mawe ya rangi ya marimari, nyekundu, nyeusi, manjano na nyeusi. Watu walipewa vinywaji katika vikombe mbalimbali vya zahabu. Na divai ya kifalme ilikuwa nyingi sawa mapato ya mufalme. Kila mutu alikunywa sawa vile alivyotaka; mufalme alikuwa ametoa maagizo kwa watumishi wa nyumba ya kifalme wamutendee kila mutu kadiri ya mahitaji yake. Wakati uleule, malkia Vashiti naye akawaandalia wanawake karamu ndani ya nyumba ya kifalme ya Ahasuero. Siku ya saba ya karamu hiyo, mufalme Ahasuero akiwa amejaa furaha kutokana na divai aliyokuwa amekunywa, akawaita matowashi saba waliomutumikia yeye mwenyewe: Mehumani, Bizita, Harbona, Bigita, Abagita, Zetari na Karkasi. Akawaamuru hao wamuletee malkia Vashiti, akiwa amevaa taji yake ya kimalkia. Malkia yule alikuwa na sura nzuri sana, hivyo mufalme alitaka kuwaonyesha wageni wake na viongozi uzuri wake. Lakini Vashiti akakataa kufika kwa amri mufalme aliyotoa kwa njia ya matowashi. Kwa hiyo, mufalme akakasirika sana na hasira yake ikawaka. Ilikuwa desturi ya mufalme kupata mashauri kutoka kwa wenye hekima, hivyo akawaita wanasheria na waamuzi kusudi wamushaurie la kufanya. Washauri wake wa kawaida walikuwa Karsena, Setari, Adimata, Tarsisi, Maresi, Marsena na Memukani – viongozi saba wa Persia na Media waliokuwa na vyeo vya juu kabisa katika utawala wake. Akawauliza hivi: “Kulingana na sheria, malkia Vashiti afanyiwe nini? Maana, nimewatuma matowashi wangu kwake, lakini yeye amekataa kuitii amri yangu, mimi mufalme Ahasuero!” Hapo Memukani akamwambia mufalme na viongozi wake: “Zaidi ya kumukosea mufalme, malkia Vashiti amewakosea viongozi na kila mutu katika majimbo ya mufalme Ahasuero! Tendo hili la malkia Vashiti litajulikana na wanawake wote, nao watawazarau waume zao, wakisema: ‘Mufalme Ahasuero aliamuru malkia Vashiti akuje kwake, lakini yeye akakataa.’ Leo hii, wanawake wa Persia na Media ambao wamesikia jinsi malkia Vashiti alivyofanya, watakuwa wanawaelezea viongozi wako; hivyo mazarau na chuki vitajaa kila pahali. Basi, ikikupendeza, ewe mufalme, toa amri kwamba Vashiti asikuje tena mbele yako. Amri hiyo iandikwe katika sheria za Persia na Media, kusudi isiweze kubadilishwa. Kisha, cheo chake cha umalkia, kipewe kwa mwanamuke mwingine anayekuwa bora zaidi kuliko yeye. Amri hiyo itakapotangazwa katika eneo lote la utawala wako, kila mwanamuke atamuheshimu mume wake, akuwe tajiri au masikini.” Wazo hilo likamupendeza sana mufalme na viongozi wake, akatimiza sawa vile Memukani alivyopendekeza. Basi, akapeleka barua kwa kila jimbo kwa luga na maandiko yanayoeleweka katika jimbo: kwamba kila mwanaume akuwe bwana wa nyumba yake, na kuitangaza habari hii kwa luga yake. Nyuma ya mambo yale, hasira yake ilipokwisha kutulia, mufalme Ahasuero akamukumbuka Vashiti, akakuwa anafikiri juu ya ugumu wake na hatua iliyokamatwa juu yake. Basi, watumishi wake, waliokuwa wanamutumikia yeye peke yake, wakamushauria: “Wamutafutie mufalme wabinti wazuri ambao ni mabikira. Mufalme achague wakubwa katika kila jimbo la utawala wake, na kuwaagiza wawalete wabinti wote wazuri ambao ni mabikira kwenye nyumba ya wanawake hapa Susani, muji mukubwa. Halafu wawekwe chini ya uangalizi wa Hegayi, towashi mwangalizi wa wanawake wako; na hapo wapewe mafuta na vifaa vingine kusudi wajipambe zaidi. Yule atakayekupendeza zaidi, afanywe malkia pahali pa Vashiti.” Mufalme akaona shauri hilo ni jema, akafanya hivyo. Katika muji wa Susani, kulikuwa mutu mumoja Muyuda, jina lake Mordekayi, mwana wa Yairi wa uzao wa Simei, na Kisi wa kabila la Benjamina. Mordekayi alikuwa kati ya watu wale waliopelekwa kuwa wafungwa wakati mufalme Yekonia wa Yuda alipotekwa na mufalme Nebukadneza wa Babeli. Alikuwa anamulea binamu yake Hadasa ndiye Esteri. Esteri alikuwa binti muzuri wa sura na umbo. Wazazi wake walipokufa, Mordekayi akamutwaa Esteri, akamulea kama binti yake. Amri ya mufalme ilipotangazwa, wabinti wengi wakapelekwa Susani, muji mukubwa, wakawekwa chini ya ulinzi wa Hegayi. Esteri naye, akapelekwa kwenye nyumba ya kifalme, akawekwa chini ya uangalizi wa Hegayi, yule mwangalizi wa wanawake. Hegayi akapendezwa na Esteri hata kiasi cha kumupendelea. Bila kupoteza wakati, akamupa Esteri mafuta na chakula. Vilevile, akamuhamishia pahali pazuri kabisa katika nyumba hiyo ya wanawake, akamuchagulia wajakazi saba kutoka nyumba ya mufalme. Esteri alikuwa hajatambulisha ukoo wala kabila lake, maana Mordekayi alikuwa amemwonya asifanye hivyo. Kila siku Mordekayi alipitapita mbele ya kiwanja cha nyumba hiyo ya wanawake kusudi apate kujua hali ya Esteri na mambo ambayo yangemupata. Kipindi cha hao wabinti kwa kujipodoa na kujitia uzuri kilikuwa mwaka mumoja: miezi sita ya kwanza walitumia mafuta ya manemane, na miezi sita ya mwisho walitumia marasi na mafuta mengine. Nyuma ya pale, kila binti, peke yake, alipelekwa kwa mufalme Ahasuero. Wakati wa kwenda kwa mufalme, kila binti alipewa kila kitu alichotaka kutwaa kutoka nyumba ya wanawake kwenda nacho katika nyumba ya kifalme. Magaribi ulikuwa ndio wakati wa kwenda, na kesho yake asubui, binti huyo alipelekwa katika nyumba nyingine ya wanawake, chini ya uongozi wa Sasagazi, towashi musimamizi wa wahabara wa mufalme. Binti hakupaswa kurudi kwa mufalme, isipokuwa kama mufalme amependezwa naye, na aliitwa kwa jina. Wakati ukafika wa Esteri kwenda kwa mufalme. Huyo, binti wa marehemu Abihaili, binamu ya Mordekayi, na ambaye alilelewa na Mordekayi, hakuomba kitu chochote zaidi ya kile alichopangiwa na Hegayi, towashi mwangalizi wa wanawake wa mufalme. Esteri akapata kukubaliwa mbele ya kila mutu aliyemwona. Basi, Esteri akapelekwa katika nyumba kwa mufalme katika mwaka wa saba wa utawala wa mufalme Ahasuero, mwezi wa kumi unaoitwa Tebeti. Mufalme akamupenda zaidi Esteri kuliko wanawake wote. Naye Esteri akapata kukubaliwa na kutendewa mema mbele yake zaidi kuliko wabinti wengine wote. Basi, mufalme akamuvalisha taji ya kimalkia kwenye kichwa, akamufanya malkia pahali pa Vashiti. Kisha mufalme akafanya karamu kubwa kwa heshima ya Esteri, akawaalika viongozi na watumishi wote wa serikali yake. Vilevile, mufalme akatangaza musamaha wa kodi katika majimbo yote, akatoa zawadi nyingi kulingana na mapato yake ya kifalme. Wabinti walipokusanyika mara ya pili, Mordekayi alikuwa anaikaa kwenye mulango wa mufalme. Esteri alikuwa bado hajatambulisha ukoo wala kabila lake kama vile Mordekayi alivyokuwa amemwonya asifanye. Naye Esteri akamutii kama alivyokuwa akimutii wakati wa utoto wake, alipolelewa naye. Wakati Mordekayi alipokuwa anaikaa kwenye mulango wa mufalme, Bigitani na Teresi, wawili kati ya matowashi wa mufalme waliokuwa walinzi wa milango ya vyumba vya mufalme, walikasirika hata wakafanya shauri baya la kumwua mufalme Ahasuero. Mordekayi akapata habari hiyo, akamujulisha malkia Esteri, naye Esteri akamupasha mufalme habari. Uchunguzi ulipofanywa, iligunduliwa kwamba ni kweli; basi, watu hao wawili wakatundikwa juu ya muti. Habari juu ya tukio hilo iliandikwa katika kitabu cha Mambo ya Siku mbele ya mufalme. Nyuma ya mambo hayo, mufalme Ahasuero akamupandisha Hamani cheo, akakuwa waziri mukubwa. Hamani alikuwa mwana wa Hamedata wa uzao wa Agagi. Mufalme akaamuru wakubwa wote wa serikali yake wamutii Hamani kwa kuinama na kupiga magoti mbele yake. Lakini Mordekayi hakuinama wala kupiga magoti mbele yake. Wakubwa mbalimbali wa mufalme waliokuwa kwenye mulango wa mufalme, wakamwuliza Mordekayi: “Mbona wewe unaizarau amri ya mufalme?” Kila siku walimushauria aache tabia hiyo, lakini Mordekayi hakukubaliana nao. Alikataa kufanya hivyo akisema kwamba yeye ni Muyuda na kwa hiyo hawezi kuinama mbele ya Hamani. Basi, wakamujulisha Hamani kusudi waone kama ataivumilia tabia ya Mordekayi. Hamani akawaka hasira alipojua kwamba Mordekayi hainami wala kupiga magoti mbele yake. Tena alipogundua kwamba Mordekayi alikuwa Muyuda, akaamua kwamba kumwazibu peke yake haitoshi. Basi akafanya shauri la kuwaangamiza Wayuda wote, watu wa ukoo wa Mordekayi, katika utawala wa mufalme Ahasuero. Katika mwaka wa kumi na mbili wa utawala wa mufalme Ahasuero, katika mwezi wa kwanza unaoitwa Nisani, wakapiga Purimu, maana yake kura, mbele ya Hamani kusudi ajue mwezi na siku ya kuwaangamiza. Basi kura ikaangukia mwezi wa kumi na mbili unaoitwa Adari. Basi, Hamani akamwambia mufalme: “Kuna watu wa taifa moja wanaokuwa kila nafasi katika utawala wako, nao wako katika kila jimbo. Watu hao wana sheria zinazokuwa tofauti kabisa na za watu wengine. Vilevile, wao hawazitii sheria zako, kwa hiyo haikufaidii kwa kitu chochote kuwavumilia. “Ikikupendeza, ewe mufalme, amri itolewe, watu hawa waangamizwe. Nami ninaahidi, kama utaamuru hivyo, nitatoa kiasi cha kilo elfu kumi za feza iwekwe katika hazina ya mufalme.” Mufalme akaivua pete yake, ambayo ilitumiwa kwa kupiga muhuri juu ya matangazo, akamupa adui wa Wayuda Hamani mwana wa Hamedata wa uzao wa Agagi. Halafu mufalme akamwambia Hamani: “Umepewa watu wote na feza zile, tumia vile unavyopenda.” Basi, siku ya kumi na tatu ya mwezi wa kwanza, Hamani akawaita waandishi wote wa mufalme, akawapa tangazo ambalo alitaka litafsiriwe kwa kila luga na kila namna ya maandiko katika utawala ule, na halafu mifano ya barua isambazwe kwa watawala wote, wakubwa wa majimbo yote, na viongozi wa makabila – kufuatana na luga zinazotumika kwao. Tangazo hilo likatolewa kwa jina la mufalme Ahasuero, na kupigwa muhuri kwa pete yake. Wajumbe wakazipeleka barua hizo kwa kila jimbo katika utawala ule. Tangazo hilo lilisema kwamba kwa siku moja tu, ni kusema siku ya kumi na tatu ya mwezi wa kumi na mbili unaoitwa Adari, Wayuda wote – tangia kwa vijana mpaka wazee, wanawake na watoto, wote wauawe, waangamizwe na kuteketezwa kabisa, na mali zao zote zinyanganywe. Barua hiyo ilitakiwa iandikwe kwa watu wote katika kila jimbo, kusudi kila mutu ajitayarishe kwa ajili ya siku hiyo. Kwa amri ya mufalme, tangazo hili lilitolewa katika muji mukubwa wa Susani, nao wajumbe wakalitangaza katika majimbo yote. Mufalme na Hamani wakaikaa chini kwa kunywa wakati watu katika muji wa Susani wanafazaika. Mordekayi alipojua yote yaliyotukia, akapasua nguo zake, akavaa nguo ya gunia, na kujitia majivu. Kisha, akapita katikati ya muji akilia kwa sauti ya uchungu. Akakwenda mpaka kwenye mulango wa nyumba ya mufalme, lakini hakuweza kuingia kwa sababu hakuna mutu aliyeruhusiwa kuingia katika nyumba ya kifalme akiwa amevaa nguo ya gunia. Katika kila jimbo, mara tu amri ya mufalme ilipotangazwa, kilio kikubwa kiliwapata Wayuda. Wakafunga, wakalia na kuomboleza; na wengi wao wakalala katika majivu wakiwa wamevaa magunia. Malkia Esteri alipoarifiwa na matowashi na wajakazi wake habari za Mordekayi akahuzunika sana. Akamupelekea Mordekayi nguo za kuvaa kwa pahali pa nguo ya gunia, lakini Mordekayi akazikataa. Basi, akamwita Hataki, mumoja wa matowashi wa mufalme aliyechaguliwa na mufalme amutumikie Esteri, akamutuma kwa Mordekayi kuuliza maneno na maana ya tukio hilo. Hataki akamwendea Mordekayi katika uwanja, mbele ya mulango wa nyumba ya kifalme. Mordekayi akamwelezea Hataki yote yaliyokuwa yamemupata, na kiasi kamili cha feza ambayo Hamani alikuwa ameahidi kulipa katika hazina ya mufalme kama Wayuda wote wangeangamizwa. Akamupa na barua moja ya tangazo lililokuwa limetolewa katika muji wa Susani juu ya kuangamizwa kwa Wayuda, akamwomba amupelekee Esteri na kumwelezea jinsi hali inavyokuwa, na kumwambia aende kumusihi mufalme na kumwomba awahurumie Wayuda, watu wa Esteri. Hataki akaenda akamwelezea Esteri maneno yote Mordekayi aliyosema. Naye Esteri akamwambia Hataki arudie amwambie Mordekayi: “Watumishi wote wa mufalme na watu wote wa majimbo yote wanajua kwamba mutu yeyote yule akiingia katika kiwanja cha ndani na kumwona mufalme bila kuitwa, huyo anapaswa kuuawa. Anayeweza kuponyoka ni yule tu ambaye mufalme atamunyooshea fimbo yake ya zahabu kwa kumuponyesha. Na mimi sijaitwa na mufalme, yapata mwezi muzima sasa.” Mordekayi alipopata ujumbe wa Esteri, akamutumia onyo hili: “Usizani kwamba kwa sababu upo katika nyumba ya kifalme wewe uko salama zaidi kuliko Muyuda mwingine yeyote. Ukikaa kimya wakati kama huu, musaada utawafikia Wayuda kutoka pahali pengine, nao wataokolewa; lakini wewe utakufa, na jamaa ya baba yako itaangamia. Ni nani anayejua pengine umefanywa kuwa malkia kwa ajili ya wakati kama huu!” Esteri akamupelekea Mordekayi jibu hili: “Kwenda uwakusanye pamoja Wayuda wote wanaokuwa katika muji wa Susani. Mufunge, musikule wala musikunywe kwa siku tatu, usiku na muchana, kwa ajili yangu. Na mimi na wajakazi wangu tutafanya vile vile. Kisha, nitamwendea mufalme, ingawa ni kinyume cha sheria. Kama ni kuuawa, niuawe.” Basi, Mordekayi akaenda zake na kufanya kama vile Esteri alivyomwambia. Kisha siku tatu ya kufunga kwake, Esteri akavaa nguo zake za kimalkia, akaenda kusimama katika kiwanja cha ndani cha nyumba ya mufalme, kuelekea chumba cha mufalme. Mufalme alikuwa mule ndani akiikaa katika kiti chake cha kifalme, kuelekea mulango wa nyumba ya mufalme. Mufalme alipomwona malkia Esteri akisimama katika kiwanja, Esteri akapata kukubaliwa mbele yake, naye akamunyooshea fimbo ya zahabu aliyokuwa akishika katika mukono wake. Esteri akakaribia, akagusa incha ya fimbo. Hapo mufalme akauliza: “Unataka nini Esteri? Uniambie unachotaka, nawe utapata – hata kama ni nusu ya ufalme wangu.” Esteri akamujibu: “Ikikupendeza, ewe mufalme, ukuje leo pamoja na Hamani, kwenye karamu ninayotayarisha kwa ajili yako, mufalme.” Mufalme akatoa amri Hamani akuje upesi, kama vile Esteri alivyoomba. Basi, mufalme na Hamani wakaenda kwenye karamu Esteri aliyotayarisha. Walipokuwa wanakunywa divai, mufalme akamwuliza tena Esteri: “Unataka nini? Uniambie, nawe utapata. Ombi lako ni nini? Hata kama ni nusu ya ufalme wangu, utapewa.” Esteri akamujibu: “Ombi langu ni hili: Kama nimepata kukubaliwa mbele yako, ewe mufalme, na ikikupendeza kukubali ombi langu, basi, ninaomba wewe na Hamani mukuje kesho kwenye karamu nyingine nitakayowaandalia. Wakati huo nitakujulisha ombi langu.” Hamani akatoka kule kwenye karamu mwenye furaha tele na moyo mukunjufu. Lakini alipomwona Mordekayi kwenye mulango wa nyumba ya kifalme, hasimami wala hamupi heshima, Hamani akawaka hasira. Hata hivyo, akajizuia, akaenda kwake. Halafu akawaalika kwake warafiki zake, na kumwomba muke wake Zeresi ajiunge nao. Halafu akaanza kueleza juu ya utajiri anaokuwa nao, wana anaokuwa nao, jinsi mufalme alivyomupandisha cheo, na jinsi alivyopewa madaraka zaidi kuliko wakubwa wengine wote wa mufalme. Hamani akaendelea kujitapa: “Vilevile malkia Esteri hakumwalika mutu mwingine yeyote pamoja na mufalme isipokuwa mimi tu. Hata kesho tena, ametualika mimi na mufalme. Lakini yote haya hayanifalii kitu ikiwa nitaendelea kumwona yule Muyuda Mordekayi kwenye mulango wa nyumba ya kifalme.” Basi, muke wake Zeresi na warafiki zake wakamushauria hivi: “Kwa nini asitengenezewe muti wa kutundikia, wenye urefu wa metre makumi mbili na mbili? Kesho asubui, unaweza kuzungumuza na mufalme kusudi Mordekayi auawe juu yake, kisha uende ukule karamu na mufalme kwa furaha.” Wazo hilo lilimufurahisha Hamani, naye akatengeneza muti ule. Usiku ule, mufalme hakupata usingizi. Basi, akaamuru kitabu cha Mambo ya Siku cha matukio ya kila siku, kiletwe, nacho kikasomwa mbele yake. Ikaonekana jinsi ilivyoandikwa ikielezwa jinsi Mordekayi alivyopasha habari ya shauri la kumwua mufalme iliyokuwa imefanywa na Bigitani na Teresi, hao wawili kati ya matowashi wa mufalme waliokuwa walinzi wa vyumba vya mufalme. Mufalme akauliza: “Tumemupa Mordekayi heshima au sifa gani kwa jambo hili?” Watumishi wake wakamujibu: “Hajafanyiwa jambo lolote.” Mufalme akauliza: “Kuna mukubwa yeyote katika kiwanja?” Ikakuwa wakati ule Hamani alikuwa ameingia katika kiwanja cha inje cha nyumba ya kifalme; alikuwa amekuja kwa mufalme kuomba Mordekayi auawe kwenye muti ambao alikuwa amekwisha kumutayarishia. Basi, watumishi wakamujibu mufalme: “Hamani yuko katika kiwanja.” Mufalme akasema: “Mumukaribishe ndani.” Hamani alipoingia ndani, mufalme akamwuliza: “Nimufanyie nini mutu ambaye ningependa sana kumupatia heshima?” Hamani akafikiri ndani ya moyo wake: “Ni nani huyo ambaye mufalme angependa kumupatia sana heshima? Bila shaka ni mimi.” Basi, Hamani akamujibu mufalme: “Mutu huyo ambaye mufalme angependa kumupatia heshima, inafaa watumishi wa mufalme walete nguo safi ya kitani mufalme aliyovaa na farasi wake mwenyewe, na mumoja wa washauri wako wa kuheshimika ee mufalme amuvalishe mutu yule nguo hizo za kifalme, na kumwongoza mutu yule akiwa amepanda juu ya farasi wako mpaka kwenye kiwanja cha muji, naye akitangaza: ‘Hivi ndivyo anavyotendewa mutu ambaye mufalme amependa kumupa heshima.’ ” Hapo mufalme akamwambia Hamani: “Fanya haraka! Twaa nguo hizi na farasi, umupatie Mordekayi heshima hii, yule Muyuda ambaye anaikaa kwenye mulango wa nyumba ya kifalme. Usiache kumufanyia hata jambo moja kati ya hayo uliyoyataja.” Basi, Hamani akatwaa nguo zile na kumuvalisha Mordekayi, akamutembeza kwenye kiwanja cha muji akiwa juu ya farasi wa mufalme, naye akitangaza: “Hivi ndivyo anavyotendewa mutu ambaye mufalme amependa kumupa heshima.” Kisha Mordekayi akarudi kwenye mulango wa nyumba ya kifalme. Lakini Hamani akakimbilia kwake, akijaa huzuni naye akifunika kichwa chake kwa ajili ya haya. Kule akawaelezea Zeresi, muke wake, na warafiki zake wote mambo yote yaliyomupata. Zeresi na hao warafiki zake wakamwambia: “Ikiwa huyu Mordekayi, ambaye umeanza kupoteza madaraka yako kwa ajili yake ni wa kabila la Wayuda, basi, hautamuweza; atakushinda kabisa.” Walipokuwa bado wanaongea juu ya hayo, matowashi wa mufalme wakafika kumutwaa Hamani kwenda kwenye karamu ya Esteri. Na hivi mufalme na Hamani wakaenda kula karamu na malkia Esteri. Katika siku ya pili, walipokuwa wanakunywa divai, mufalme akamwuliza tena Esteri: “Sasa, malkia Esteri, unataka nini? Uniambie, nawe utapata. Ombi lako ni nini? Hata kama ni nusu ya ufalme wangu, utapewa.” Malkia Esteri akamujibu: “Kama nimepata kukubaliwa mbele yako, ewe mufalme, na ikikupendeza kunitimizia ombi langu, hitaji yangu ni mimi niishi na watu wangu vilevile. Maana, mimi na watu wangu tumeuzishwa kusudi tuuawe, tuangamizwe na kuteketezwa kabisa. Kama tungeuzishwa tu kuwa watumwa na wajakazi, ningekaa kimya wala nisingekusumbua. Ingawa tutateswa hakuna adui atakayeweza kulipa hasara hii kwa mufalme.” Hapo mufalme Ahasuero akamwuliza malkia Esteri: “Ni nani huyo anayesubutu kufanya jambo kama hilo? Yuko wapi mutu huyo?” Esteri akamujibu: “Adui yetu mukubwa na mutesaji wetu, ni huyu mwovu Hamani!” Hapo Hamani akashikwa na hofu mbele ya malkia na mufalme. Mufalme akasimama kwa hasira, akatoka ndani ya chumba kwenye karamu ya divai na kwenda inje kwenye bustani ya nyumba ya kifalme. Hamani alipoona kwamba mufalme amekusudia kumwazibu, akabaki nyuma kwa kumusihi malkia Esteri ayaponyeshe maisha yake. Kisha mufalme akarudi kutoka katika bustani, na mara alipoingia ndani ya chumba walimokuwa wanakunywa divai, akamukuta Hamani amejitupa karibu na kiti ambamo Esteri alikuwa ameikaa. Kuona hivyo, mufalme akasema kwa sauti kubwa: “Hivi mutu huyu anataka kumushika kwa nguvu malkia mbele yangu, tena ndani ya nyumba ya kifalme?” Mara tu mbele mufalme hajamaliza kusema, matowashi wakamufunika Hamani uso. Harbona, mumoja wa wale matowashi waliomutumikia mufalme, akasema: “Hamani amesubutu hata kutengeneza muti wa kumutundikia Mordekayi ambaye aliyaokoa maisha yako, ewe mufalme. Muti huo, wenye urefu wa metre makumi mbili na mbili, bado uko kule katika nyumba yake.” Hapo mufalme akaamuru: “Mumutundike Hamani juu ya muti uleule.” Naye, Hamani akauawa pale kwenye muti aliokuwa amemutayarishia Mordekayi. Basi, hasira ya mufalme ikapoa. Siku ileile, mufalme Ahasuero akamupatia malkia Esteri mali yote ya Hamani, adui ya Wayuda. Esteri akamujulisha mufalme kwamba Mordekayi ni ndugu yake. Basi, tangu wakati ule, Mordekayi akaruhusiwa kumwona mufalme. Mufalme akaivua pete yake ya muhuri aliyokuwa amemunyanganya Hamani, akamupa Mordekayi. Esteri naye akamupa Mordekayi mamlaka juu ya mali ya Hamani. Kisha Esteri akazungumuza tena na mufalme; akajitupa chini, kwenye miguu ya mufalme, naye akilia, akamusihi mufalme aukomeshe mupango mubaya ambao Hamani, wa uzao wa Agagi, alikuwa amepanga juu ya Wayuda. Mufalme akamunyooshea Esteri fimbo yake ya zahabu, naye Esteri akasimama na kusema: “Ikikupendeza, ewe mufalme, na kama nimepata kukubaliwa mbele yako, ukiona ni vizuri nami nikikupendeza, tafazali, toa tangazo la kuvunja mipango ambayo Hamani alikuwa ameamuru itimizwe. Mipango hiyo ni ile ya mwana wa Hamedata, wa uzao wa Agagi, aliyopanga kwa kuwaangamiza Wayuda wote katika majimbo yote. Maana, ninaweza namna gani kuvumilia kuona watu wangu wanaangamizwa na wandugu zangu wanauawa?” Mufalme Ahasuero akawaambia malkia Esteri na Mordekayi, yule Muyuda: “Muangalie! Nimemupa Esteri mali ya Hamani, naye wamekwisha kumutundika kwa sababu ya shauri lake baya juu ya Wayuda. Munaweza kuwaandikia Wayuda neno lolote munalopenda. Tena munaweza kuandika kwa jina langu na kutumia muhuri wa kifalme, kwa sababu tangazo ambalo limetolewa kwa jina la mufalme na kupigwa muhuri wa mufalme, haliwezi kuvunjwa.” Basi, katika siku ya makumi mbili na tatu ya mwezi wa tatu inayoitwa Siwani, Mordekayi akawaita waandishi wote wa mufalme, akawaagiza waandike barua kwa Wayuda na wakubwa, watawala na wakubwa wa majimbo yote mia moja makumi mbili na saba, kuanzia Uhindi mpaka Etiopia. Barua hizo zikaandikwa kwa kila jimbo katika luga yake na sawasawa na maandiko yake, vilevile na kwa Wayuda kwa maandiko yao na luga yao. Mordekayi alikuwa ameandika barua hizo kwa jina la mufalme Ahasuero, akazipiga muhuri kwa pete ya mufalme. Na waliozipeleka walikuwa wajumbe waliopanda juu ya farasi wenye nguvu wanaokimbia mbio. Kwa njia ya barua hizi mufalme akawaruhusu Wayuda katika kila muji kukusanyika kwa kuyalinda maisha yao. Walikuwa na ruhusa ya kuharibu, kuua bila huruma na kuangamiza kundi lolote la watu au jimbo, lenye kuwashambulia kwa silaha pamoja na wanawake na watoto wao, na kunyanganya mali zao. Jambo hili lingefanyika katika majimbo yote ya mufalme Ahasuero, katika siku ya kumi na tatu ya mwezi wa kumi na mbili, ni kusema Adari. Mifano ya tangazo hili ambalo lilitolewa kama sheria katika kila jimbo ilisambazwa kwa kila mutu katika kila jimbo, kusudi Wayuda wajitayarishe kulipiza kisasi siku hiyo itakapofika. Kwa amri ya mufalme, wajumbe waliopanda juu ya farasi wa kifalme wenye nguvu wanaokimbia mbio, wakaondoka mbio. Tangazo hili vilevile lilitolewa katika muji mukubwa Susani. Mordekayi alipotoka katika nyumba kwa mufalme, akiwa amevaa nguo ya kifalme ya rangi ya mayungiyungi na nyeupe, koti la kitani safi la rangi nyekundu, na taji kubwa ya zahabu, muji wa Susani ukajaa shangwe na vigelegele. Hapo Wayuda wakapata utukufu, heshima na furaha, wakajisikia wenye shangwe na ushindi. Katika kila jimbo na kila muji, popote pale tangazo hili liliposomwa, Wayuda wakafurahi na kushangilia, wakafanya sherehe na mapumziko; na watu wengine wengi wakajifanya kuwa Wayuda, maana waliwaogopa sana Wayuda. Siku ya kumi na tatu ya mwezi wa kumi na mbili, ni kusema mwezi wa Adari, ilipofika, siku ambayo tangazo la mufalme lingetimizwa, na waadui za Wayuda walitarajia kuwashinda Wayuda, ikageuzwa kuwa siku ya ushindi kwa Wayuda juu ya waadui zao. Katika kila muji wa kila jimbo wa mufalme Ahasuero, Wayuda walijitayarisha vizuri kumushambulia mutu yeyote ambaye angejaribu kuwazuru. Nao viongozi wote wa majimbo, watawala, wakubwa na wakubwa wa mufalme vilevile waliwasaidia Wayuda, maana wote walimwogopa Mordekayi. Mordekayi sasa akakuwa mutu mwenye madaraka makubwa katika nyumba ya kifalme, na habari zake zikaenea katika majimbo yote kwamba uwezo wake ulikuwa unazidi kuongezeka. Basi, Wayuda wakawashambulia waadui zao kwa upanga, wakawachinja, wakawaangamiza na kuwatendea kama walivyopenda. Kule katika muji wa Susani, Wayuda waliwaua watu mia tano. Vilevile waliwaua Parsandata, Dalfoni, Asipata, Porata, Adalia, Aridata, Parmasta, Arisayi, Aridayi na Wayezata, wana kumi wa Hamani mwana wa Hamedata, adui ya Wayuda. Hata hivyo, hawakunyanganya mali zao. Siku ileile, mufalme akajulishwa jumla ya watu waliouawa katika muji mukubwa wa Susani. Halafu mufalme akamwambia malkia Esteri: “Katika muji mukubwa peke yake Wayuda wamewaua watu mia tano, pamoja na wana kumi wa Hamani. Unafikiri wamefanya nini kule katika majimbo! Unataka nini sasa? Maana utatimiziwa. Uniambie, unataka nini zaidi, nawe utapewa.” Esteri akasema: “Ikikupendeza, ewe mufalme, kesho uwaruhusu Wayuda wanaokuwa Susani wafanye kama agizo la leo lilivyokuwa. Tena, uamuru wana kumi wa Hamani watundikwe kwenye miti.” Mufalme akaamuru hayo yatimizwe, na tangazo likatolewa katika muji Susani. Wana kumi wa Hamani wakatundikwa juu ya muti. Siku ya kumi na ine ya mwezi wa Adari, Wayuda wakakusanyika tena, wakawaua watu mia tatu zaidi katika muji wa Susani. Lakini hawakunyanganya mali za watu. Wayuda waliokuwa katika majimbo nao vilevile wakajitayarisha kuyalinda maisha yao. Wakaokolewa kutoka kwa waadui zao, wakawaua watu yapata elfu kumi na tano, lakini hawakunyanganya mali zao. Siku hiyo ilikuwa ya kumi na tatu ya mwezi wa Adari. Siku iliyofuata ya kumi na ine, wakapumzika, wakaifanya kuwa siku ya karamu na sherehe. Lakini Wayuda wa muji mukubwa wa Susani wakakusanyika vilevile siku ya kumi na ine lakini hawakupumzika. Walisherehekea siku ya kumi na tano kwa furaha na shangwe. Kutokana na sababu hii, Wayuda wanaokaa katika vijiji na katika miji midogo wanasherehekea siku ya kumi na ine ya mwezi wa Adari kuwa sikukuu ya furaha, na kupelekeana zawadi wakati wale wanaoishi katika miji mikubwa wanasherehekea siku ya kumi na tano ya mwezi wa Adari kama siku ya mapumziko, na kupelekeana vilevile zawadi. Mordekayi aliandika mambo haya yote. Kisha akaandika barua kwa Wayuda wote waliokuwa katika utawala wa Ahasuero. Aliwaonya kila mwaka washike sikukuu, siku ya kumi na ine na siku ya kumi na tano ya mwezi wa Adari. Wayuda walishinda waadui zao katika siku hizo, na katika mwezi huo huzuni yao iligeuzwa kuwa furaha, na kilio chao kuwa sikukuu. Waliagizwa wakuwe wanazikumbuka siku hizo kwa kufanya karamu na sherehe, kupelekeana zawadi za chakula na kuwapa wamasikini vitu. Basi, Wayuda wakakubaliana kufanya kama walivyoanza na kama vile Mordekayi alivyowaandikia. Hamani mwana wa Hamedata wa ukoo wa Agagi na adui wa Wayuda alikuwa amefanya mupango juu ya Wayuda kwa kuwaangamiza, vilevile alikuwa amepiga purimu, ni kusema kura, kwa kuamua siku ya kuwaponda na kuwaangamiza Wayuda. Lakini Esteri alipomwendea mufalme, naye mufalme akatoa amri kwa waandishi kwamba lile shauri baya ambalo Hamani alikuwa amefanya juu ya Wayuda, limurudilie yeye mwenyewe; na ya kuwa yeye na wana wake wauawe kwa kutundikwa kwenye muti. Kwa hiyo, wakaita siku hizo Purimu, kutokana na neno puri maana yake kura. Kwa sababu ya barua ya Mordekayi na mambo waliyoyaona wenyewe na yale yaliyowapata, Wayuda wakaifanya kuwa sheria kwao, kwa wazao wao na kwa mutu yeyote ambaye angejiunga nao, kwamba katika wakati uliopangwa kila mwaka, bila kukosa, siku hizo mbili zishikwe kulingana na maagizo ya Mordekayi. Vilevile walikubaliana kwamba kila jamaa ya Kiyuda, kizazi kwa kizazi, katika kila jimbo na muji, sharti ikumbuke siku za Purimu na kuzisherehekea siku zote. Halafu malkia Esteri, binti ya Abihaili, akaandika barua kwa mamlaka yake yote, pamoja na Mordekayi Muyuda kuhakikisha ile Mordekayi aliyoiandika pale mbele juu ya Purimu. Barua ile iliandikwa kwa Wayuda wote, na mifano ya barua zile kupelekewa katika majimbo yote mia moja makumi mbili na saba ya ufalme wa Ahasuero. Barua ile iliwatakia Wayuda amani na usalama, na kuwaamuru wao na wazao wao washike sikukuu za Purimu kwa wakati wake uliopangwa, kama vile walivyokuwa wanazikumbuka sheria za kufunga wakati wa kuomboleza. Maagizo haya yalitolewa na Mordekayi, Muyuda, pamoja na malkia Esteri. Amri ya Esteri ikahakikisha mambo hayo ya Purimu; ikaandikwa katika kitabu. Mufalme Ahasuero alilipisha kodi kwa watu wa inchi na katika visanga vya bahari. Matendo yake yote makubwa na ya ajabu, pamoja na simulizi kamili juu ya jinsi alivyomupandisha Mordekayi cheo na kumupatia heshima kubwa, yote yameandikwa katika kitabu cha Mambo ya Siku cha ufalme wa Media na Persia. Mordekayi, Muyuda, alikuwa wa kwanza chini ya mufalme Ahasuero katika madaraka. Alipendwa na kuheshimiwa na Wayuda, maana alitumika kwa faida na amani ya watu wake na wazao wao wote. Kulikuwa mutu mumoja katika inchi ya Usi, aliyeitwa Yobu. Mutu yule alikuwa mukamilifu, wa usawa, mwenye kumwogopa Mungu na mwenye kuepukana na uovu. Yobu alikuwa na wana saba na wabinti watatu. Alikuwa na mali, kondoo elfu saba, ngamia elfu tatu, ngombe elfu moja, punda dike mia tano, na watumishi wengi sana. Yeye alikuwa wa heshima kuliko watu wote kule upande wa mashariki. Mara kwa mara, wana wa Yobu walifanya karamu katika nyumba ya kila mumoja wakifuatana. Waliwaalika wadada zao kula na kunywa pamoja nao. Kila mara karamu ilipomalizika, Yobu aliita wana wake kusudi awatakase. Aliamuka asubui mapema kisha karamu, akatoa sadaka za kuteketezwa kwa moto kwa ajili ya kila mumoja wao maana aliwaza: “Labda wana wangu wametenda zambi na kumutukana Mungu ndani ya mioyo yao.” Basi, ikatukia siku moja wamalaika wa Mungu walikwenda kukutana mbele ya Yawe. Shetani akakuja kuwa pamoja nao. Yawe akamwuliza Shetani: “Unatoka wapi wewe?” Shetani akamujibu Yawe: “Ninatoka kutembeatembea na kuzungukazunguka katika dunia.” Yawe akamwambia Shetani: “Umemwona vizuri mutumishi wangu Yobu? Katika dunia hakuna mwingine anayekuwa kama yeye. Yeye ni mutu mukamilifu, wa usawa, mwenye kumwogopa Mungu na mwenye kuepukana na uovu.” Shetani akamujibu Yawe: “Yobu anamwogopa Yawe kwa bure? Si wewe mwenyewe unamulinda pande zote pamoja na jamaa yake na kila kitu anachokuwa nacho? Wewe umemubariki na mali yake imeongezeka katika inchi. Lakini sasa, unyooshe mukono wako uguse mali yake. Utaona namna atakutukana waziwazi!” Yawe akamwambia Shetani: “Basi, unaweza kufanya vile unavyotaka juu ya mali yake. Lakini tu yeye mwenyewe usimuguse.” Basi, Shetani akaondoka mbele ya Yawe. Siku moja, wana na wabinti wa Yobu walikuwa wanakula na kunywa divai pamoja katika nyumba ya kaka yao mukubwa. Basi, mutumishi akafika kwa Yobu, akamwambia: “Tulikuwa tunalima kwa majembe ya kukokotwa na ngombe. Punda nao walikuwa wanakula pale karibu. Basi Wasabea wakatushambulia na kunyanganya nyama na kuua watumishi kwa upanga. Ni mimi tu peke yangu nimepona kwa kuja kukuletea habari.” Alipokuwa hajamaliza kusema, mwingine akafika, akasema: “Umeme wa radi umewachoma na kuwateketeza kondoo na watumishi. Ni mimi tu peke yangu nimepona kwa kuja kukuletea habari.” Yule naye alipokuwa hajamaliza kusema, mwingine akafika, akasema: “Wakaldea walijipanga makundi matatu, wakashambulia ngamia, wakawatwaa, na wakaua watumishi wako kwa upanga! Ni mimi tu peke yangu nimepona kwa kuja kukuletea habari.” Alipokuwa hajamaliza kusema, mwingine akakuja, akasema: “Wana zako na wabinti zako walikuwa wanakula na kunywa divai katika nyumba ya kwa kaka yao mukubwa. Mara moja upepo mukali ukavuma kutoka katika jangwa, ukaipiga nyumba ile kila upande nayo ikawaangukia, na vijana wote wamekufa. Ni mimi tu peke yangu nimepona kwa kuja kukuletea habari.” Kisha Yobu akasimama, akapasua nguo yake, akanyoa nywele zake, akajitupa chini na kumwabudu Mungu, akisema: Nilikuja uchi katika dunia, nitaondoka uchi katika dunia. Yawe amenipa, Yawe ametwaa. Jina la Yawe litukuzwe. Katika mambo haya yote Yobu hakutenda zambi wala hakumushitaki Mungu kuwa na kosa. Ikatokea tena siku ingine, wamalaika wa Mungu walikwenda kukutana mbele ya Yawe. Shetani akakuja kuwa pamoja nao. Yawe akamwuliza Shetani: “Unatoka wapi wewe?” Naye Shetani akamujibu Yawe: “Ninatoka kutembeatembea na kuzungukazunguka katika dunia.” Yawe akamwambia Shetani: “Umemwona vizuri mutumishi wangu Yobu? Katika dunia hakuna mwingine anayekuwa kama yeye. Yeye ni mutu mukamilifu, wa usawa, mwenye kumwogopa Mungu na mwenye kuepukana na uovu. Yeye anadumu katika ukamilifu, ingawa wewe umenisukuma nimwangamize bure.” Shetani akamujibu Yawe: “Ngozi kwa ngozi! Mutu anatoa kila kitu anachokuwa nacho kusudi aokoe maisha yake. Lakini sasa, unyooshe mukono wako umuguse mwili wake. Utaona namna atakutukana waziwazi.” Yawe akamwambia Shetani: “Basi, unaweza kumufanya vile unavyotaka, lakini usimwue tu.” Kwa hiyo Shetani akaondoka mbele ya Yawe, akamutesa Yobu kwa vidonda vikali tangia kwenye miguu yake mpaka kwenye kichwa chake. Yobu akatwaa kigae, akajikuna nacho na kuikaa kwenye majivu. Muke wake akamwambia: “Unaendelea kushikilia ukamilifu wako? Umutukane Mungu, ukufe.” Akamujibu: “Wewe unasema kama wanawake wapumbafu. Tukipokea mazuri kutoka kwa Mungu, kwa nini tukatae kupokea vilevile mabaya kutoka kwake?” Katika mambo hayo yote, Yobu hakusema neno lolote la kumukosea Mungu. Warafiki watatu wa Yobu walisikia juu ya hasara zote zilizomupata Yobu, wakaamua kwa pamoja waende kumupa pole na kumufariji. Majina yao ni: Elifasi kutoka inchi ya Temani, Bildadi wa inchi ya Suhi na Zofari wa inchi ya Namati. Walipomwona kwa mbali hawakumutambua. Basi, wakaanza kulalamika na kulia. Wakapasua nguo zao, wakarusha mavumbi katika anga na juu ya vichwa vyao. Kisha wakaikaa kwenye udongo pamoja na Yobu kwa siku saba, muchana na usiku, bila kumwambia neno lolote maana waliona mateso yake kuwa makubwa sana. Kisha hayo, Yobu akaamua kusema. Akalaani siku aliyozaliwa. Yobu akasema: Iangamie siku ile niliyozaliwa, usiku ule iliposemwa: “Mimba ya mutoto mwanaume imepatikana.” Siku ile ikuwe giza! Na kutoka juu Mungu asijishugulishe nayo, wala mwangaza wowote usiiangaze! Itawaliwe na giza kubwa sana, mawingu mazito yaifunike. Giza la muchana liitishe! Usiku ule giza kubwa liufunike! Usihesabiwe katika siku za mwaka, usitiwe katika hesabu ya siku za mwezi. Usiku ule ukuwe tasa, sauti ya furaha isiingie ndani yake. Ulaaniwe na wale wanaolaani siku, wale wafundi wanaoamusha Leviatani. Nyota zake za mapambazuko zififie, utamani kupata mwangaza, lakini usipate, wala usione mwangaza wa mapambazuko. Usiku ule ukuwe hivi, kwa sababu haukufunga tumbo la mama, wala kuficha taabu nisizione. Kwa nini sikukufa nilipozaliwa? Kwa nini kutoka tu katika tumbo sikutoweka? Kwa nini mama yangu alinizaa? Kwa nini nilipata kunyonya? Maana ningekuwa nimezikwa, kimya; ningelala na kupumzika pamoja na wafalme na watawala wa dunia waliojijengea upya miji kutoka mabomoko, pamoja na wakubwa waliokuwa na zahabu, waliojaza nyumba zao feza tele. Kwa nini sikukuwa kama mutoto aliyezaliwa mufu ambaye hakuona mwangaza? Kule kwa wafu waovu hawasumbui mutu, kule wanaochoka wanapumzika. Kule wafungwa wanastarehe pamoja, hawasikii hata kidogo sauti ya wasimamizi. Wakubwa na wadogo wako kule, nao watumwa wamepata uhuru mbali na bwana zao. Kwa nini kumujalia mwangaza na uzima yule anayekuwa katika taabu, anayekuwa na huzuni ndani ya moyo, anayetamani kifo lakini hakufi, anayetafuta kifo kuliko hazina iliyofichwa. Mutu kama yule atashangilia sana na kufurahi atakapokufa na kuzikwa! Kwa nini kumujalia uzima mutu ambaye njia zake zimefungwa, mutu ambaye Mungu amemwekea kizuizi? Kuugua ndicho chakula changu. Malalamiko yangu yanatiririka kama maji. Kile ninachoogopa kimenipata; ninachohofu ndicho kilitokea. Sina amani wala utulivu; sipumziki, taabu imenifikia. Kisha Elifasi wa inchi ya Temani akamujibu Yobu: Mutu akijaribu kukuambia neno utakasirika? Lakini nani anayeweza kujizuia kusema? Sikiliza! Wewe umewafundisha wengi, na kuiimarisha mikono ya wazaifu. Maneno yako yamewainua moyo, umewaimarisha waliokosa nguvu. Lakini sasa shida imekupata nawe unaregea. Imekugusa, nawe unafazaika. Kumwogopa Mungu si ndilo tegemeo lako? Na ukamilifu wa mwenendo wako si ndilo tumaini lako? Fikiri sasa: nani asiyekuwa na kosa ambaye amepata kuangamia? Au, watu wa usawa wamepata kutupiliwa? Mimi nimeona kwamba wanaopanda uovu na ubaya wanavuna yaleyale. Mungu anawaangamiza kwa pumzi yake; wanateketezwa kwa kuvuma kwa hasira yake. Waovu wananguruma kama simba mukali, lakini meno yao inavunjwa. Simba mwenye nguvu anakufa kwa kukosa chakula, na watoto wa simba dike wanatawanywa! Siku moja, niliambiwa neno kwa siri, sikio langu lilisikia manongonezo yake. Ilikuwa usiku wakati watu wanapoota ndoto, wakati usingizi muzito unawashika watu. Nikashikwa na hofu na kutetemeka; mifupa yangu yote ikagonganagongana. Upepo ukapita mbele ya uso wangu, nywele za mwili wangu zikasimama. Kitu kimoja kikasimama mbele yangu. Nilipokiangalia sikukitambua kabisa. Kulikuwa umbo moja mbele yangu. Kulikuwa kimya, kisha nikasikia sauti: “Mwanadamu anaweza kuwa mwenye haki mbele ya Mungu? Mutu anaweza kuwa safi mbele ya Muumba wake? Mungu hawaaminie hata watumishi wake, na wamalaika wake anawaona wana kosa. Zaidi sana wanadamu, viumbe vya udongo, watu ambao musingi wao ni mavumbi, ambao wanaweza kupondwapondwa kama chawa! Wanadamu wanaangamia kwa saa chache tu; wanaangamia milele bila kuacha hata alama. Kama uzi unaoshikilia uzima wao ukikatwa, wao wanakufa, tena bila kuwa na hekima”. Ita sasa, uone kama kuna wa kukuitikia. Ni nani kati ya watakatifu utakayemwita? Kweli mahangaiko yanamwua mupumbafu, na wivu unamwangamiza mujinga. Nimepata kuona mupumbafu akistawi, lakini kwa rafla nikalaani makao yake. Watoto wake hawana usalama. Wanaonelewa katika tribinali, na hakuna mutu wa kuwatetea. Mazao yake yanakuliwa na wenye njaa, hata ngano iliyoota kati ya miiba. Wenye tamaa wananyanganya utajiri wake. Kwa kawaida mateso hayatoki katika mavumbi, wala matatizo hayachipuki katika udongo. Lakini mwanadamu anazaliwa apate taabu, kama vile cheche za moto zinavyoruka juu. Kwa ngambo yangu, mimi ningemugeukia Mungu, ningemutolea Mungu maneno yangu, yeye anayetenda mambo makubwa yasiyochunguzika, anayetenda maajabu yasiyohesabika. Ananyeshea inchi mvua, anapeleka maji katika mashamba. Anainua juu wanaokuwa zaifu; wenye kuomboleza anawapa usalama. Anavunja mipango ya wadanganyifu, matendo yao yasipate mafanikio. Anawanasa wenye hekima kwa werevu wao, anakomesha mara moja mipango ya waovu. Wao wanapatwa na giza wakati wa muchana; muchana kati wanapapasapapasa kama vile usiku. Lakini Mungu anawaokoa wayatima wasiuawe, anawaponyesha wakosefu toka katika mikono ya wenye nguvu. Hivyo wamasikini wanapata tumaini, nao uovu unakomeshwa. Heri mutu yule anayeazibiwa na Mungu! Hivyo usizarau Mungu Mwenye Uwezo anapokuazibu. Maana yeye anaumiza na tena anatunza, anatia kidonda na kwa mukono wake anaponyesha. Atakuokoa mara sita toka katika magumu; hata mara saba hasara haitakugusa. Atakuepusha toka kifo wakati wa njaa, toka mapigo ya upanga wakati wa vita. Utakingwa salama na mashambulio ya ulimi, wala hautaogopa maangamizi yanapokuja. Maangamizi na njaa vinapokuja, utacheka, wala hautaogopa nyama wakali wa inchi. Nawe utapatana na mawe ya shamba, na nyama wakali watakuwa na amani nawe. Utakaa na amani katika nyumba yako; utachunguza makundi yako ya nyama, utaona yote iko. Utaona vilevile wazao wako watakuwa wengi, wengi kama majani katika mashamba. Utashuka katika kaburi ukiwa na miaka yenye kutimia, kama vile muganda wa ngano uliokomaa vizuri. Basi haya ndiyo mambo tuliyochunguza. Ni hivi tu. Uyasikie na kuyaelewa kwa faida yako. Yobu akamujibu Elifasi: Heri uchungu wangu ungepimwa, nayo mateso yangu yote yangewekwa katika mizani! Yangekuwa mazito kuliko muchanga wa bahari. Ni kwa hiyo maneno yangu hayana maana! Mishale ya Mungu Mwenye Uwezo imenichoma; nafsi yangu imekunywa sumu yake. Vitisho vya Mungu vimenipata. Punda wa pori analia akiwa na majani, au ngombe akiwa na malisho? Kitu kisichokuwa na onjo kinaweza kuliwa bila chumvi? Sehemu nyeupe ya yai ina utamu wowote? Sina hamu ya kuvigusa vyakula hivyo, hivyo ni vyakula vinavyonichukiza. Heri ningejibiwa kwa ombi langu, Mungu angenipatia kile ninachotamani, angependezwa kunipondaponda, angenyoosha mukono wake juu yangu na kuniua! Hiyo ingekuwa faraja yangu, ningefurahi katika maumivu yasiyokuwa na huruma, kwa sababu sikukataa maagizo ya Mungu Mutakatifu. Sina nguvu ya kuweza kuendelea. Sijui mwisho wangu utakuwa namna gani, nipate kuvumilia. Nguvu zangu ni kama za mawe? Au mwili wangu kama shaba? Kweli kwangu hakuna kitu cha kunisaidia; musaada wowote ni mbali nami. Anayekataa kutendea mema rafiki yake, anakataa kumwogopa Mungu Mwenye Uwezo. Warafiki zangu wamenidanganya kama kijito, wamenidanganya kama mifereji isiyokuwa na maji, ambayo imejaa barafu, na teluji imejificha ndani yake. Wakati wa kipwa inatoweka, wakati wa jua kali inakauka. Wasafiri wanapotea njia zao wakitafuta maji, wanapanda katika jangwa na kukufia kule. Wasafiri toka Tema wanatafutatafuta, wasafiri toka Sheba wanatumainia. Wanachukizwa kwa kutumainia bure, wanafika kwenye vijito hivyo na kuuzika. Ninyi mumekuwa kama vijito hivyo, munaona hasara yangu na kuogopa. Nimesema munipe zawadi? Au munitolee sehemu ya mali zenu? Au muniokoe toka katika mikono ya adui? Au munikomboe toka katika mukono wa watesaji? Munifundishe, nami nitanyamaza. Munieleweshe jinsi nilivyokosa. Maneno ya kweli yana nguvu kubwa! Lakini makaripio yenu yanafaa kwa nini? Munazani kwamba munaweza kuchunguza maneno? Maneno ya mutu aliyekata tamaa ni upepo tu. Ninyi munasubutu hata kuwapigia wayatima kura; munauzisha hata rafiki yenu! Lakini sasa muniangalie tafazali. Mimi sitasema uongo mbele yenu. Tafazali mugeuke, kusikuwe uovu; muache sasa, kwa ajili ya haki yangu. Munazani kwamba nimesema uovu? Munafikiri kwamba mimi siyatambui machungu? Mwanadamu ana magumu katika dunia, na siku zake ni kama siku za mutumishi wa mushahara! Yeye ni kama mutumwa anayetamani kivuli, kama mutumishi anayengoja kwa hamu mushahara wake. Basi nimepangiwa miezi na miezi ya taabu, urizi wangu ni kuteseka usiku kwa usiku. Ninapolala ninasema: “Nitaamuka wakati gani?” Maana saa za usiku ni ndefu sana; ninagaagaa katika kitanda mpaka mapambazuko! Mwili wangu umejaa vidudu na uchafu; ngozi yangu imekauka na kutokwa na usaha wa jipu. Siku zangu zinapita mbio kuliko gurudumu la mushonaji, nazo zinafikia mwisho wake bila matumaini. Kumbuka, maisha yangu ni pumzi tu; jicho langu halitaona jambo zuri lolote tena. Anayeniona sasa, hataniona tena, mara tu ukiniangalia nitakuwa nimetoweka. Kama vile wingu linavyofifia na kutoweka, ndivyo nao watu wanavyoshukia kuzimu bila kurudi. Anayeondoka harudi tena kwa jamaa yake, na pale alipokuwa anaishi, wanamusahau mara moja. Kwa hiyo sitakizuia kinywa changu kusema. Nitasema kwa kusongwa kwa roho yangu, nitalalamika kwa uchungu wa nafsi yangu. Mimi ni bahari au nyama mukubwa wa bahari hata upate kuniwekea mulinzi? Nikisema “Kitanda kitanipumzisha, matandiko yangu yatanipunguzia malalamiko yangu”, wewe unakuja kunitia hofu kwa ndoto, unanitisha kwa kuniletea maono, hata ninaona afazali kutundikwa, ninaona heri kufa kuliko kupata mateso haya. Ninayachukia maisha yangu. Sitaishi milele. Muniache, maana siku zangu ni pumzi tu! Mwanadamu ni nini hata umujali? Kwa nini unajishugulisha naye na kuja kumuchunguza kila asubui, na kumupima kila wakati? Utaendelea kuniangalia mpaka wakati gani, bila kuniacha hata nimeze mate? Kama nikitenda zambi, inakuuzi nini, ewe muchungaji wa wanadamu? Mbona umeniweka kuwa shabaha ya mapigo yako? Kwa nini nimekuwa muzigo kwako? Mbona haunisamehe kosa langu na kuniondolea uovu wangu? Hivi kisha muda kidogo nitalazwa chini katika mavumbi. Utanitafuta, lakini sitakuwa tena! Halafu Bildadi wa inchi ya Suhi akamujibu Yobu: Utasema mambo haya mpaka wakati gani? Mpaka wakati gani maneno yako yatakuwa matupu kama upepo? Maana, unazani Mungu anapotosha sheria? Au, Mungu Mwenye Uwezo anapotosha haki? Kama watoto wako wamemukosea Mungu, yeye amewalipiza matokeo ya makosa yao. Kama utamutafuta Mungu na kumusihi yule Mungu Mwenye Uwezo, kama wewe uko safi ndani ya moyo na wa usawa, kweli Mungu atakuja kukusaidia, na kukujalia makao unayostahili. Na ingawa ulianza kuishi kwa uzaifu, maisha yako ya mwisho yatakuwa bora zaidi. Tafazali, ujifunze kwa wale waliotutangulia; shika mambo ambayo wazee walitambua. Sisi ni watu wa juzijuzi tu, hatujui kitu; siku zetu katika dunia ni kivuli kinachopita. Lakini wao watakufundisha na kukuambia mambo waliyopata kuyatoa katika maarifa yao. Nyasi zinaota tu penye tingitingi, matete yanastawi pahali panapokuwa maji. Hata kama yamechanua na bila kukatwa, yakikosa maji yananyauka mbele ya mimea mingine. Ndivyo wote wanaomusahau Mungu wanavyokuwa. Tumaini la wasiomwamini Mungu litapotea. Tegemeo lao linavunjika, tumaini lao ni utando wa buibui. Wanaegemea nyumba yao lakini haitasimama, wanaishikilia lakini haidumu. Wako kama ua ambalo jua linapotoka linastawi; linaeneza matawi yake katika bustani yake, mizizi yake inajisokotasokota kwenye mawe, nalo linaenda kuchunguza ndani ya jiwe. Lakini likiangamizwa kutoka makao yake, hayo yatalikana yakisema: “Sijakuona bado.” Ile ndiyo furaha ya mwisho wake, na pahali pake patachipuka mengine. Sikia! Mungu hatakataa mutu mukamilifu, wala hatasaidia waovu. Lakini atajaza kinywa chako kicheko, na midomo yako sauti ya furaha. Wale wanaokuchukia watapata haya, makao ya waovu yatatoweka kabisa. Kisha Yobu akajibu: Kweli ninajua kama ni hivi. Lakini mutu anaweza namna gani kuwa haki mbele ya Mungu? Kama mutu angesubutu kushindana naye, hataweza kufika mbali, hata kujibu ulizo moja kati ya elfu. Yeye ni mwenye hekima sana na nguvu nyingi. Nani aliyepingana naye, akashinda? Yeye anahamisha milima bila yenyewe kutambua, anaipindua mbali kwa hasira yake. Yeye anaitikisa dunia kutoka pahali pake, na nguzo zake zinatetemeka. Anaamuru jua lisipande, anafunika nyota zisiangaze. Yeye peke yake alitandaza mbingu, na kuyakanyaga mawimbi ya bahari. Yeye aliweka makundi ya nyota katika anga: Dubu, Orioni, Kilimia, na Vyumba vya Kusini. Ndiye anayetenda mambo makubwa yasiyoeleweka, mambo ya ajabu yasiyokuwa na hesabu. Anapita karibu nami lakini simwoni, kisha anajiendea zake bila mimi kumutambua. Yeye akitwaa kitu kwa rafla, nani anayeweza kumuzuia? Nani anayeweza kumwuliza: “Unafanya nini?” Mungu hatazuia hasira yake; Rahabu na wasaidizi wake wanainama chini mbele yake. Nitaweza namna gani basi kumujibu Mungu? Nitachagua wapi maneno ya kumwambia? Ingawa sina kosa, siwezi kumujibu. Ninapaswa kumwomba mwamuzi wangu huruma. Hata kama ningemwita naye akijibu, nisingeweza kuamini kwamba ananisikiliza. Yeye ananiponda kwa zoruba, anaongeza vidonda vyangu bila sababu. Haniachi hata nipumue; maisha yangu anayajaza uchungu. Kama ni kushindana, yeye ana nguvu sana! Na kama ni kutafuta juu ya haki, nani atakayemuleta mbele ya tribinali? Ingawa sina kosa, maneno yangu yenyewe yangenihukumu. Ingawa mimi ni mukamilifu, yangehakikisha kwamba mimi ni mupotovu. Mimi ni mukamilifu. Siangalii nafsi yangu. Ninachukia maisha yangu. Yote ni mamoja, kwa hiyo ninasema: Mungu anawaangamiza wakamilifu na waovu. Musiba unapoleta kifo cha rafla, anachekelea hasara ya wasiokuwa na kosa. Inchi ikitiwa katika utawala wa mwovu, Mungu anafunga macho ya waamuzi wake! Kama si yeye anayefanya hivyo, ni nani basi? Siku zangu zinaenda mbio kuliko mukimbiaji, zinakimbia bila kuona faida. Zinapita mbio kama mashua ya matete, kama tai anayerukia mawindo yake. Ninasema: “Nitasahau malalamiko yangu, niondoe uso wangu wa huzuni na kuwa na furaha!” Lakini ninaogopa maumivu yangu yote, maana ninajua Mungu hataniona kuwa sina kosa. Ikiwa nitahukumiwa kuwa na kosa, kwa nini basi nijisumbue bure? Hata kama nikinawa na teluji, na kujitakasa mikono kwa sabuni, hata hivyo, atanitumbukiza katika shimo kwenye uchafu, na nguo zangu zitanichukia. Mungu si mutu kama mimi nipate kumujibu, hata tuweze kwenda katika tribinali pamoja. Hakuna mwamuzi kati yetu ambaye angetuamua sisi wawili. Mungu aniondolee hiyo fimbo ya kunipiga, na kitisho chake kisinitie hofu! Halafu ningeweza kusema bila kumwogopa; maana si vile ninavyokuwa ndani yangu. Ninachukia maisha yangu! Malalamiko yangu nitayasema bila kizuizi. Nitasema kwa uchungu wa moyo wangu. Nitamwambia Mungu: Usinitendee sawa na mwenye makosa. Unijulishe sababu ya kugombana nami. Ni sawa kwako kunionea, kuzarau kazi ya mikono yako na kupendelea mipango ya waovu? Uko na macho kama ya mwanadamu? Unaona kama vile mwanadamu anavyoona? Siku zako ni kama za mwanadamu? Miaka yako kama ya mwanadamu? Kwa nini unachunguza uovu wangu na kuitafuta zambi yangu? Wewe unajua kwamba mimi sina kosa, na hakuna wa kuniokoa toka katika mikono yako. Mikono yako ilinitengeneza na kuniumba, lakini sasa unageuka kwa kuniangamiza. Kumbuka kwamba uliniumba kwa udongo. Utanirudisha tena katika mavumbi? Si wewe uliyenimimia kama maziwa, na kunigandisha kama siagi? Uliuumba mwili wangu kwa mifupa na mishipa, ukaifunika mifupa yangu kwa nyama na ngozi. Ukanipa uzima na kunitendea mema, ukalinda nafsi yangu kwa uangalifu. Hata hivyo mambo haya uliyaficha ndani ya moyo. Lakini ninajua kwamba ile ilikuwa nia yako. Ulikuwa unangojea uone kama nitatenda zambi, kusudi ukatae kunisamehe uovu wangu. Kama mimi ni mwovu, ole wangu! Kama mimi ni mwenye haki, siwezi kujisifu; maana nimejaa haya, nikiangalia mateso yangu. Nikiinua kichwa tu, unaniwinda kama simba na kuniponda tena kwa maajabu yako. Kila mara uko na ushuhuda juu yangu, unaongeza hasira yako juu yangu, unaniletea waadui wapya wanishambulie. Ee Mungu, kwa nini ulinitoa katika tumbo ya mama? Afazali ningekufa mbele ya watu kuniona, ningepelekwa katika kaburi, na kuwa kama mutu asiyekuwa. Siku za maisha yangu si chache? Uniachilie nipate kufurahi kidogo, mbele ya kwenda kule ambako sitarudi, kule kwenye inchi ya huzuni na giza kubwa; inchi ya huzuni na fujo, ambako mwangaza wake ni kama giza. Kisha Zofari wa inchi ya Namati akamujibu Yobu: Wingi huu wa maneno uachwe tu bila kujibiwa? Mutu wa maneno mengi anaonyesha kwamba hana kosa? Kupapayuka kwako kutanyamazisha watu? Kama ukichekelea watu, hakuna atakayekupatisha haya? Wewe unasema: “Masemi yangu ni safi, mimi sina kosa mbele ya Mungu.” Heri Mungu angefungua kinywa chake na kutoa sauti yake kwa kukujibu! Angekuelezea siri za hekima, maana yeye yuko na maarifa mengi. Ujue kwamba Mungu hakuhesabu makosa yako yote. Unaweza kuvumbua siri za Mungu na kujua ukomo wa Mungu Mwenye Uwezo? Ukubwa wake unapita mbingu; wewe unaweza nini? Kimo chake kinapita kuzimu; wewe unaweza kujua nini? Ukubwa ule unapita urefu wa dunia, unapita upana wa bahari. Kama Mungu akipita, akimufunga mutu na kumuhukumu, nani anayeweza kumuzuia? Mungu anajua watu wasiofaa; anaona uovu vilevile bila magumu. Mupumbafu hawezi kuwa na maarifa. Punda wa pori ni punda wa pori tu. Yobu, ukifanya moyo wako mukamilifu, utainua mikono yako kwa kumwomba Mungu! Kama uovu uko katika mukono wako, uutupilie mbali. Usikubali ubaya ukuwe katika nyumba yako. Halafu utainua uso wako bila kosa, utakuwa imara bila kuwa na hofu. Utazisahau taabu zako zote; utazikumbuka tu kama mafuriko yaliyopita. Maisha yako yataangaa kuliko jua la muchana kati, giza lake litabadilika kuwa mapambazuko. Utakuwa na uhakika maana kuna tumaini; utalindwa na kupumzika salama. Utalala bila kuogopeshwa na mutu; watu wengi watakuomba musaada. Lakini waovu macho yao yatafifia, njia zote za kutorokea zitawapotea; tumaini lao la mwisho ni kukata roho! Halafu Yobu akajibu: Hakika! Ninyi ni watu wa hekima. Hekima itakufa wakati ule mutakapokufa. Mimi nami nina ufahamu kama ninyi. Mimi si mutu wa akili ndogo kuliko ninyi. Yote muliyosema kila mutu anajua. Nilikuwa mutu wa kumwomba Mungu na kupata jibu lake. Sasa, watu wananichekelea. Wanachekelea mutu mukamilifu, mwenye haki. Mutu mwenye raha anazarau taabu; taabu ni kwa wale wanaoteleza. Makao ya wanyanganyi yana amani. Wenye kumuchokoza Mungu wako salama; nguvu yao ni mungu wao. Lakini uulize nyama nao watakufundisha; uulize ndege nao watakuambia. Au uulize mimea nayo itakufundisha; sema na samaki nao watakuarifu. Nani kati ya viumbe hivyo, asiyejua kwamba Yawe ametenda yale? Uzima wa kila kiumbe, pumzi ya kila mwanadamu, viko katika mikono yake. Sikio halipimi maneno kama vile ulimi unavyoonja chakula? Hekima iko kwa watu wazee, maarifa kwa walioishi muda murefu. Lakini hekima na uwezo ni vya Mungu. Yeye ana maarifa na ujuzi. Akibomoa, hakuna anayeweza kujenga upya; akifunga mutu, hakuna anayeweza kumufungua. Akizuia mvua, inchi inakauka; akiifungulia, inchi inaharibika. Yeye ana nguvu na hekima. Wanaodanganywa na wanaodanganya ni wake. Anawatembeza washauri miguu wazi, anawafanya waamuzi kuwa wapumbafu. Anavua wafalme mikaba yao, na kuwafunga kamba za wafungwa katika viuno. Anaacha makuhani watembee uchi; na kuwaangusha wenye nguvu. Ananyanganya washauri zawadi yao ya kusema, anaondolea wazee ufahamu wao. Anamwagia wakubwa mazarau, anawaondolea wenye uwezo nguvu yao. Anafunua vilindi vya giza, na kuleta katika mwangaza mambo yaliyokuwa katika giza. Anayaongeza mataifa kisha anayaangamiza, anayafanya yapanuke kisha anayatawanya. Anaondolea viongozi wa watu ujuzi wao, anawafanya watangetange katika jangwa kusikokuwa njia, wakipapasapapasa katika giza kusikokuwa mwangaza; na kuwafanya wapepesuke kama walevi. Sikia! Hayo yote nimeyaona kwa macho yangu. Nimeyasikia kwa masikio yangu mwenyewe na kuelewa. Yote munayoyajua, mimi vilevile ninayajua. Mimi si mutu wa akili ndogo kuliko ninyi. Lakini ningependa kusema na Mungu Mwenye Uwezo, ninatamani kujitetea mbele ya Mungu. Lakini ninyi munapakaa uongo chokaa, ninyi wote ni waganga wasiofaa kitu. Heri mungekaa kimya kabisa, muonekane kwamba muna hekima! Musikilize basi utetezi wangu, munisikilize ninapojitetea. Munazani munamutumikia Mungu kwa kusema uongo na udanganyifu? Munajaribu kumupendeza Mungu? Mutamutetea Mungu katika tribinali? Akiwachunguza, ninyi mutapona? Au munazani munaweza kumudanganya Mungu kama watu? Hakika yeye atawakaripia kama mukionyesha upendeleo kwa siri. Utukufu wake hauwatishi? Hamupatwi na hofu juu yake? Masemi yenu ni mezali za majivu, maneno yenu ni ukuta wa udongo. Munyamaze, nami niseme. Kitu kitakachonipata, kinipate. Niko tayari hata kuhatarisha maisha yangu. Mungu aniue akitaka; sina la kupoteza. Hata hivyo nitautetea mwenendo wangu mbele yake. Kama nikiweza kwa hiyo nitakuwa nimeshinda, maana mutu mwovu hawezi kwenda mbele yake. Musikilize kwa uangalifu maneno yangu, maelezo yangu yatue katika masikio yenu. Maneno yangu nimeyatarisha jinsi inavyofaa. Ninajua kwamba sina kosa. Nani atakayebishana nami? Niko tayari kunyamaza na kufa. Mungu wangu, unijalie tu mambo haya mawili, nami sitajificha mbali na wewe: kwanza uniondolee mukono wako unaonipiga, na usiniogopeshe kwa kitisho chako. Uanze kusema maneno yako nami nikujibu. Au mimi nianze, nawe unijibu. Makosa na zambi zangu ni ngapi? Unijulishe kosa na zambi yangu. Mbona unageuza uso wako mbali nami? Kwa nini unanitendea kama adui yako? Utatikisatikisa jani linalopeperushwa, au kukimbiza nyasi iliyokauka? Wewe umetoa mashitaki makali juu yangu, na kunibebesha zambi za ujana wangu. Unanifunga minyororo kwenye miguu, unachunguza njia zangu zote, umeichapa miguu yangu. Nami ninaisha kama muti uliooza, kama nguo iliyokuliwa na nondo. Mutu anazaliwa na mwanamuke, ana siku chache, na taabu nyingi. Anachanua kama maua, kisha ananyauka. Anakimbia kama kivuli na kutoweka. Ee Mungu, kwa nini unajali hata kumwangalia na kuanza kusamba naye? Nani anayeweza kutoa kitu kisafi kutoka kitu kichafu? Hakuna anayeweza. Siku za kuishi za mwanadamu zimepimwa. Ee Mungu, umepanga hesabu ya miezi yake; hawezi kupita mupaka uliomwekea. Angalia pembeni basi, umwache, kusudi apate kufurahia siku zake kama mutumishi wa mushahara. Muti ukikatwa, kuna tumaini la kuota, unaweza kuchipuka tena. Japo mizizi yake itazeeka katika udongo, na shina lake kukufia ndani ya udongo, lakini kwa harufu tu ya maji utachipuka, utatoa matawi kama chipukizi. Lakini mutu anakufa na ule ndio mwisho wake. Akisha kutoa roho, anabakiliwa na nini tena? Kama vile maji yanavyokauka katika ziwa, na muto unavyokoma kutiririka, ndivyo mutu anavyokufa, wala haamuki tena. Hataamuka tena wala kusisimuka, hata pale mbingu zitakapotoweka. Heri ungenificha katika kuzimu, ungenificha mpaka kasirani yako itulie, nawe ungenipimia muda kwa kunikumbuka tena. Mutu akikufa anaweza kuishi tena? Siku zangu zote za kazi ningekungoja mpaka wakati wa kufunguliwa ufike. Halafu ungeniita, nami ningeitika, wakati ungetaka kuniona mimi kiumbe chako. Kwa hiyo ungeweza kuhesabu hatua zangu, ungeacha kuchunguza zambi zangu. Makosa yangu yangefungiwa katika mufuko, nawe ungefunika uovu wangu. Lakini milima inaanguka nayo mawe yanaongoka pahali pake. Mitiririko wa maji inakulakula mawe, mvua kubwa inaleta mumomonyoko wa udongo. Ndivyo nawe unavyoharibu tumaini la mwanadamu. Wewe unamwangusha mwanadamu, naye anatoweka milele; unaubadilisha uso wake na kumutupilia mbali. Watoto wake wakiheshimika, yeye hana habari. Wakizarauliwa, yeye haoni kabisa. Anasikia tu maumivu ya mwili wake, na kuomboleza tu hali yake mbaya. Kisha Elifasi wa inchi ya Temani, akajibu: Mwenye hekima anajibu bila kufikiri na kujaa maneno ya burebure? Anajitetea kwa maneno yasiyofaa na yasiyokuwa na maana? Lakini wewe, woga wa Mungu si ndani yako; nawe unakataa kufikiri mbele ya Mungu. Uovu wako ndio unaongoza kinywa chako, nawe unachagua kusema kama wadanganyifu. Maneno yako mwenyewe yanakuhukumu, sio mimi; masemi yako yanashuhudia juu yako. Wewe ndiwe mutu wa kwanza kuzaliwa? Wewe ulizaliwa mbele ya kuwa kwa vilima? Ulipata kuwa katika shauri la Mungu? Wewe ndiwe peke yako mwenye hekima? Unajua kitu gani tusichokijua sisi? Unafahamu kitu gani tusichokifahamu sisi? Kati yetu kuna wazee wenye hekima, wenye miaka mingi kuliko baba yako. Faraja Mungu anazokupa ni ndogo sana? Au neno lake la upole kwako si kitu? Mbona moyo unakusukuma kukasirika na kutoa macho makali, hata kumwasi Mungu na kusema maneno mabaya kama yale? Mutu ni nini hata aweze kuwa na moyo safi? Yule aliyezaliwa na mwanamuke atapata kuwa mwenye haki? Ikiwa Mungu hawaaminii hata wamalaika wake, nazo mbingu si safi mbele yake, kefu sasa mwanadamu anayekuwa chukizo na mupotovu, mwanadamu anayetenda uovu kama kunywa maji! Sasa unisikilize, nami nitakuonyesha, nitakuambia yale niliyoona, mafundisho ya wenye hekima, mambo ambayo wazee wao hawakuficha, ambao Mungu aliwapa hiyo inchi peke yao, wala hakuna mugeni aliyepita kati yao. Mwovu atateseka kwa maumivu siku zote, miaka yote watesaji waliyopangiwa. Sauti za vitisho zitamupigia kelele katika masikio. Anapozani amestawi, mwangamizi atamushambulia. Mwovu hana tumaini la kutoka katika giza; mwisho wake ni kufa kwa upanga. Anatangatanga kutafuta chakula, akisema: “Kiko wapi?” Anajua kwamba siku ya giza inamukaribia. Taabu na uchungu, vinamutisha; vinamushambulia kama jeshi la mufalme anayekuwa tayari kwa vita kwa sababu amenyoosha mukono wake apigane na Mungu na kujivuna kumupinga yule Mungu Mwenye Uwezo. Anakimbia kwa kiburi kwa kumushambulia, akiwa na ngao yenye mafundo makubwa. Uso wake umenona kwa mafuta, na kiuno chake kimenenepa. Ameishi katika miji iliyoachwa wazi, katika nyumba zisizokaliwa na mutu, nyumba zilizotakiwa zikuwe lundo la uharibifu. Mutu yule hatakuwa tajiri hata kidogo; wala utajiri wake hautadumu katika dunia. Hataponyoka giza la kifo. Ndimi za moto zitakausha vichipukizi vyake, maua yake yatapeperushwa na upepo. Aache kutumainia udanganyifu, maana udanganyifu ndio utakaokuwa zawadi yake. Atalipwa kikamilifu mbele ya kufa kwake, na wazao wake hawatadumu. Atakuwa kama muzabibu unaoangusha zabibu mbichi, kama muzeituni unaopoteza maua yake. Wote wasiomwogopa Mungu hawatapata watoto, moto utateketeza mahema ya wanaokula kituliro. Wanatunga udanganyifu na kuzaa uovu. Mioyo yao inapanga udanganyifu. Halafu Yobu akajibu: Mambo kama yale nimeyasikia mengi; ninyi ni wafariji wenye kutaabisha! Mwisho wa maneno haya ya bure ni wakati gani? Au ni kitu gani kinachowasukuma kujibu? Kama mungekuwa mimi, na mimi ninyi, ningeweza kusema kama ninyi. Ningeweza kutunga maneno juu yenu, na kutikisa kichwa changu. Ningeweza kuwatia moyo kwa maneno yangu, na maneno yangu ya faraja yangewatuliza. Lakini nikisema maumivu yangu hayatulii, na nikikaa kimya hayaondoki. Kweli Mungu amenichakalisha, ameharibu kila kitu karibu nami. Amenifanya ninyauke na huo ni ushuhuda juu yangu. Kukonda kwangu kumenishitaki na kushuhudia juu yangu. Amenirarua kwa hasira na kunichukia, amenisagia meno, na adui yangu ananitonolea macho. Watu wanafungua vinywa vyao na kunichekelea. Makundi kwa makundi wananizunguka na kunipiga makofi kwenye mashavu. Mungu amenitia katika mikono ya wapotovu na kunitupa katika mikono ya waovu. Nilikuwa nimestarehe, lakini akanivunjavunja. Alinikamatia katika shingo na kunipasua vipandevipande. Akanifanya shabaha ya mishale yake, akanipiga mishale kutoka kila upande. Amenipasua figo bila huruma, na nyongo yangu akaimwanga chini. Ananivunja na kunipiga tena na tena; ananishambulia kama askari. Nimejishonea nguo za gunia; utukufu wangu nikautupa katika mavumbi. Macho yangu ni mekundu kwa sababu ya kulia, kope zangu zimekuwa nyeusi sana, ingawa sijatesa watu kwa mukono wangu, na maombi yangu kwa Mungu ni safi. Ewe dunia, usifunike damu yangu iliyomwangika; kilio changu kienee kila pahali. Nina uhakika kwamba nina mushuhuda wangu mbinguni; mwenye kunitetea yuko kule juu. Warafiki zangu wanizarau; ninatoa machozi kumwomba Mungu. Heri mutu angenitetea mbele ya Mungu, kama vile inavyofanyika katika dunia kati ya watu wawili. Kweli, miaka yangu ni michache, nami nitakwenda kule ambako sitarudi. Nimevunjika moyo, siku zangu zimekwisha, kaburi langu liko tayari. Kweli wanaonichekelea wamenizunguka, matusi yao yananizuiza kulala. Ee Mungu, ujitoe mwenyewe kuwa rehani kwa ajili yangu maana hakuna mwingine wa kujitoa kwa ajili yangu. Umefumba akili za warafiki zangu; usiwaache basi wanishinde. Mutu anayefitini warafiki zake kwa faida, watoto wake watakufa macho. Nimefanywa kuwa kichekesho kwa watu, nimekuwa mutu wa kutemewa mate. Macho yangu yamefifia kwa ajili ya uchungu; viungo vyangu vyote vimekuwa kama kivuli. Watu wa haki wanashangaa wanapoona hayo, nao wasiokuwa na kosa wanachukizwa na wasiomwogopa Mungu. Hata hivyo, mutu wa haki anashika njia yake, mutu ambaye hajafanya ubaya kwa mukono wake anazidi kuwa na nguvu. Lakini ninyi mukuje, mukuje wote tena. Kwenu sitamupata mwenye hekima hata mumoja. Siku zangu zimekwisha, mipango yangu imevunjwa, matazamio ya moyo wangu yametoweka. Kwa hao watu, usiku ni muchana: wanasema kwamba mwangaza unakaribia giza. Kama kuzimu kukiwa nyumba yangu, na makao yangu yako kule katika giza, kama nikiita kaburi “baba yangu” na vidudu “mama yangu” au “dada yangu”, basi, nimebakiliwa na tumaini gani? Ni nani anayeweza kuona tumaini lile? Tazamio langu litashuka nami kuzimu! Tutateremuka wote wawili mpaka kule katika mavumbi! Kisha Bildadi, wa inchi ya Suhi, akajibu: Utawinda maneno ya kusema mpaka wakati gani? Fikiri vizuri nasi tutasema. Kwa nini unatufanya kama ngombe? Mbona unatuona sisi kuwa wapumbafu? Wewe unajirarua mwenyewe kwa hasira zako. Dunia itaachwa tupu kwa ajili yako au mawe yahamishwe toka pahali pake? Kweli, mwangaza wa mutu mwovu utazimishwa; ulimi wa moto wake hautaangaa. Katika nyumba yake mwangaza ni giza, taa inayomwangazia itazimishwa. Hatua zake ndefu zitafupishwa; mipango yake itamwangusha chini. Miguu yake mwenyewe itamutia katika mutego; kila mara anatembea juu ya shimo. Mutego unamukamata kwenye kisigino, kamba inamunasa kabisa. Amefichiwa kamba ya kumunasa ndani ya udongo, ametegewa mutego katika njia yake. Hofu kubwa inamutisha kila upande, inamufuata katika kila hatua yake. Alikuwa na nguvu, lakini sasa njaa imemubana; hasara ziko tayari kumwangusha. Ugonjwa mukali unakula ngozi yake, ugonjwa wa kifo unaharibu viungo vyake. Anaongolewa katika nyumba aliyotegemea, na kupelekwa kwa mufalme wa vitisho. Nyumba yake tupu, wengine wataishi ndani; kiberiti kimetawanywa katika makao yake. Yeye ni kama muti uliokauka mizizi, matawi yake juu yamenyauka. Katika inchi hakuna atakayemukumbuka; jina lake halitatamkwa tena katika barabara. Ameondolewa toka katika mwangaza, akatupwa katika giza; amefukuzwa mbali kutoka katika dunia. Hana watoto wala wajukuu; hakuna aliyebaki katika makao yake. Watu wa upande wa magaribi wameshangazwa na yaliyomupata; hofu imewapata watu wa upande wa mashariki. Hayo ndiyo yanayowapata wasiomujali Mungu; pale ndipo pahali pa wasiomujua Mungu. Kisha Yobu akajibu: Mutaendelea kunitesa mpaka wakati gani, na kunivunjavunja kwa maneno? Mara hizi zote kumi mumenitukana. Basi, hamusikii haya kunitendea vibaya? Hata kama ingekuwa nimekosa kweli, kosa langu linanielekea mimi mwenyewe. Munaishusha hali yangu mupate kujipandisha; munanitusi kwa kunyenyekezwa kwangu. Mujue kwamba Mungu amenitendea vibaya na kuninasa katika wavu wake. Ninalalamika: “Mateso makali!” lakini sijibiwi. Ninaita kwa sauti kubwa, lakini sipati haki yangu. Njia yangu ameiziba kwa ukuta kusudi nisipite, njia zangu amezitia giza. Amenivua utukufu wangu; ameiondoa taji yangu juu ya kichwa. Amenivunja pande zote, nami nimekwisha; tumaini langu ameliongoa kama muti. Ameichochea kasirani yake juu yangu; ameniona kuwa kama adui yake. Majeshi yake yananifikia kwa pamoja; yametengeneza njia ya kuja kwangu, yamepiga kambi kuizunguka nyumba yangu. Mungu amewaweka wandugu zangu mbali nami; warafiki zangu wakubwa wamenitoroka kabisa. Wandugu zangu na warafiki hawanisaidii tena. Wageni katika nyumba yangu wamenisahau; wajakazi wangu wananiona kuwa mugeni. Mimi nimekuwa kwao mutu wasiyemujua. Ninamwita mutumishi wangu lakini haitikii, ninalazimishwa kumusihi sana kwa maneno. Nimekuwa harufu mbaya kwa muke wangu; chukizo kwa wandugu zangu wa tumbo. Hata watoto wadogo wananizarau; wakati ninapojitokeza wao wananizomea. Warafiki zangu wakubwa wanachukizwa nami, wale niliokuwa nikiwapenda wamenigeuka. Mwili wangu umebakia tu mifupa na ngozi, nimeponyoka kisha kupoteza yote. Munionee huruma, munionee huruma, enyi warafiki zangu; maana mukono wa Mungu umenigusa. Kwa nini munanifuatilia kama Mungu? Mbona hamutosheki na mwili wangu? Heri maneno yangu yangeandikwa! Heri yangeandikwa katika kitabu! Heri yangechorwa kwa chuma na risasi juu ya jiwe kusudi yadumu! Ninajua wazi Mukombozi wangu anaishi. Kwa mwisho yeye atasimama hapahapa katika dunia. Na nyuma ngozi yangu kuharibika hivyo, nitamwona Mungu nikiwa na mwili huu. Mimi mwenyewe nitakutana naye. Mimi mwenyewe na si mwingine nitamwona kwa macho. Moyo wangu unachomwa kwa kumungojea. Ninyi munaweza kujisemesha: “Tutamufuatilia namna gani? Namna gani tutapata kwake maneno ya kumushitaki?” Lakini muogope azabu, chuki yenu isiwaletee kifo. Mujue kwamba kutakuwa hukumu! Kisha Zofari wa inchi ya Namati akajibu: Mafikiri yangu yananisukuma nikujibu, wala siwezi kujizuia tena. Ninasikia maonyo nisiyoweza kuvumilia, lakini akili yangu inanisukuma nijibu. Wewe labda umesahau jambo hili: kwamba tangu zamani Mungu alipomwumba mutu katika dunia, mwovu atajiona ameshinda kwa muda tu, furaha ya asiyemwogopa Mungu ni ya muda mufupi tu! Mwovu akiweza kupanda hata kufikia mbingu, na kichwa chake kufika kwenye mawingu, atatupiliwa mbali kama mavi yake. Waliopata kumujua watajiuliza: “Yuko wapi?” Atatoweka kama ndoto, asionekane tena, atafutikana kama maono ya usiku. Aliyemwona, hatamwona tena, wala pale alipoishi hapatatambuliwa tena. Yeye mwenyewe atarudisha mali yake yote, watoto wake wataomba huruma kwa wamasikini. Japo alijisikia amejaa nguvu ya ujana, lakini italala pamoja naye katika mavumbi. Katika kinywa chake uovu ni mutamu kama sukari, anauficha chini ya ulimi wake; hataki kabisa kuuachilia, lakini anaushikilia katika kinywa chake. Lakini unapofika ndani ya tumbo unakuwa muchungu, mukali kama sumu ya nyoka. Mwovu anameza mali haramu na kuitapika; Mungu anaitoa ndani ya tumbo lake. Ananyonya sumu ya nyoka na nyoka atamuuma na kumwua. Hataona tena mitiririko ya asali na ya maziwa. Ataacha matunda ya jasho lake. Hatakuwa na uwezo wa kuyaonja, kwa sababu amewaangamiza wamasikini na kuwaachilia, amenyanganya nyumba ambazo hakuzijenga. Kwa vile ulafi wake hauna mwisho, hataweza kuokoa kitu chochote cha lazima. Kisha kula hakuacha hata makombo. Kwa hiyo fanaka yake yote haitadumu. Atakapotajirika sana atapatwa na taabu, hasara itamupata kwa nguvu zote. Akiwa anajishugulisha kwa kushibisha tumbo, Mungu atamuletea kasirani yake imutiririkie kama chakula chake. Labda ataweza kuepuka upanga wa chuma, kumbe atachomwa na upanga wa shaba. Mushale utachomolewa kutoka katika mwili wake; incha yake itatolewa katika mugongo wake ikingaa, vitisho vya kifo vitamupata. Hazina zake zitaharibiwa, moto wa ajabu utamuteketeza; kilichobaki katika nyumba yake kitateketezwa. Mbingu zitafichua uovu wake, dunia itajitokeza kumushambulia. Mali zake zitanyanganywa katika siku ya kasirani ya Mungu. Hii ndiyo sehemu ya mutu mwovu kutoka kwa Mungu, ndio mwisho aliopangiwa na Mungu. Kisha Yobu akajibu: Musikilize kwa uangalifu maneno yangu; na hiyo ikuwe ndiyo faraja yenu. Munivumilie, nami nitasema, na nikisha sema muendelee kunichekelea. Basi, mimi ninamulalamikia mwanadamu? Kwa nini basi nikose uvumilivu? Muniangalie, nanyi mushangae, muweke mikono yenu juu ya vinywa vyenu. Nikifikiri yaliyonipata ninafazaika, mwili wangu unatetemeka kwa hofu. Kwa nini waovu wanaendelea kuishi? Mbona nguvu zao zinaongezeka hata katika uzee? Wanaona watoto wao wakifanikiwa na wazao wao wakipata nguvu. Kwao kila kitu ni salama bila hofu, wala fimbo ya Mungu haiwafikii. Kweli, ngombe wao wote wanaongezeka, wanazaa bila matatizo yoyote. Watoto wao wachanga wanatembea kama kundi; na watoto wao wanacheza ngoma; wanacheza muziki wa ngoma na vinubi, na kufurahia sauti ya filimbi. Wanaishi maisha ya fanaka kisha wanashuka kwa amani katika kuzimu. Wanamwambia Mungu: “Usitusumbue! Hatutaki kujua mapenzi yako. Mungu Mwenye Uwezo ni nini hata tumutumikie? Tunapata faida gani tukimwomba?” Kufanikiwa kwao si kuko katika mikono yao, wakiwa wamemuweka Mungu mbali na mipango yao? Mara ngapi umepata kuona mwangaza wa maisha ya mwovu umezimishwa na kupatwa na hasara? Au Mungu amekwisha kuwaangamiza kwa hasira yake? Hata hivyo, wapeperushwe kama majani yenye kukauka, wakuwe kama maganda yanayopelekwa na zoruba! Ninyi munasema: “Mungu amewawekea watoto wao azabu ya watu wale waovu.” Kwa nini hawalipizi wao wenyewe, wapate kutambua? Waone wenyewe maangamizi yao; waone wenyewe kasirani ya Mungu Mwenye Uwezo. Maana siku zao zitakapokwisha, watajali nini juu ya wazao wao? Mwanadamu anaweza kumufundisha Mungu maarifa, Mungu ambaye anahukumu wakaaji wa mbinguni? Mutu mumoja anakufa mwenye nguvu tele, akiwa katika raha na salama, akijaa mafuta tele katika mwili, na mifupa yake ikiwa bado na nguvu. Mwingine anakufa na huzuni kubwa ndani ya moyo, akiwa hajaonja bado jambo lolote jema. Hata hivyo, wote wanakufa na kuzikwa, wote wanafunikwa na vidudu. Musikilize! Mimi ninajua mawazo yenu yote, na mipango yenu ya kunizarau. Ninyi munauliza: “Iko wapi nyumba ya yule mukubwa? Iko wapi nyumba mwovu alimoishi?” Hamujawauliza wapita njia? Hamukufahamu habari zao? Mwovu anaponyeshwa siku ya hasara, anaokolewa siku ya kasirani! Ni nani atakayemwonyesha makosa yake, au atakayemulipa kwa yote aliyotenda? Anapokamatwa kupelekwa katika kaburi, kaburi lake linalindwa. Nyuma yake watu wengi wanamusindikiza na wengine wengi sana wanamutangulia. Anapozikwa, udongo unateremushwa polepole. Mutaweza namna gani basi, kunifariji kwa maneno matupu? Majibu yenu hayana kitu chochote lakini uongo tu. Kisha Elifasi wa inchi ya Temani akajibu Yobu: Mwanadamu anafaa kwa kitu chochote mbele ya Mungu? Kwa kweli mwenye hekima anajifaidia mwenyewe tu. Unazani kwamba unamufurahisha Mungu Mwenye Uwezo kama wewe ni mwenye haki? Au anapata faida gani kama uko mukamilifu? Unazani anakuazibu na kukuhukumu kwa sababu wewe unamuheshimu? Hapana! Uovu wako ni mukubwa sana! Ubaya wako hauna mwisho! Wewe umemunyanganya ndugu yako nguo ya rehani; umemutwaa nguo hiyo moja anayokuwa nayo. Umewanyima maji wale waliokuwa wamechoka; umewanyima chakula wale wanaokuwa na njaa. Umemuruhusu mwenye cheo kunyanganya inchi yote; umemwacha anayependelewa aishi mule. Umewaacha wajane waende mikono mitupu; umewaponda wayatima mikono yao. Kwa hiyo mitego imekuzunguka pande zote, hofu ya rafla imekupata. Giza limekuangukia usione kitu; mafuriko ya maji yamekufunika. Tunajua kwamba Mungu yuko kule juu mbinguni; Angalia jinsi nyota za juu kabisa zinavyokuwa mbali! Lakini wewe unasema: “Mungu anajua nini? Anaweza kupenya mawingu na kutoa hukumu? Mawingu mazito yamemuzunguka asipate kuona; anatembea inje ya anga la dunia!” Umeamua kufuata njia za zamani ambazo watu waovu wamezifuata? Hao walifagiliwa mbele ya wakati wao, misingi yao imepelekwa mbali na maji. Hao ndio waliomwambia Mungu: “Achana nasi!” Na “Wewe Mungu Mwenye Uwezo unaweza nini juu yetu?” Lakini Mungu ndiye aliyejaza nyumba zao fanaka, lakini walimuweka mbali na mipango yao! Wenye haki wanaona na kufurahi, wasiokuwa na kosa wanawachekelea. Wanasema: kweli wale waadui zetu wameangamizwa, na walichoacha kimeteketezwa kwa moto. Sasa, Yobu, ukubaliane na Mungu ukuwe na amani, na kwa hiyo mazuri yatakufikia. Pokea mafundisho kutoka kwake; na uyaweke maneno yake ndani ya moyo wako. Ukimurudilia Mungu na kunyenyekea, ukiondoa uovu mbali na makao yako, ukitupilia mbali mali yako, ukitupa zahabu ya Ofiri kwenye ukingo wa kijito, Mungu Mwenye Uwezo akiwa ndiyo zahabu yako na feza yako ya bei kali, basi, ndipo utakapomufurahia Mungu Mwenye Uwezo na kuinua uso wako kwake. Utamwomba naye atakusikiliza, nawe utavitimiza viapo vyako. Neno lolote utakalokusudia litafanikiwa, na mwangaza utaangazia njia zako. Maana, Mungu anawashusha wenye majivuno, lakini anawaokoa wanyenyekevu. Yeye anamwokoa mutu asiyekuwa na kosa. Nawe utaokolewa kwa sababu haukutenda mabaya. Kisha Yobu akajibu: Hata leo malalamiko yangu ni ya uchungu. Ninapata maumivu na kuugua. Heri ningejua pahali nitakapomupata Mungu! Ningeweza kwenda hata karibu naye. Ningeleta maneno yangu mbele yake, na kumutolea utetezi wangu. Ningeweza kujua atakachonijibu, na kuelewa atakachoniambia. Angeshindana nami kwa nguvu zake zote? Hapana! Bila shaka angenisikiliza. Pale, mutu wa usawa anaweza kujitetea. Mungu, mwamuzi wangu angeamua kuwa sina kosa milele. Ninakwenda mbele, lakini simupati; ninarudi nyuma, lakini siwezi kumwona. Ninamutafuta upande wa kushoto lakini simwoni; ninageukia upande wa kuume, lakini siwezi kumwona. Lakini yeye anajua njia ninayofuata; atakapomaliza kunipima nitatoka mule safi kama zahabu. Ninamufuata kabisa; njia yake nimeishikilia wala sikugeuka pembeni. Sijaacha hata kidogo kushika amri yake; maneno yake nimeyatunza ndani ya moyo wangu. Lakini yeye habadiliki, nani anayeweza kumugeuza? Kitu anachotaka, ndicho anachofanya! Anatimiza yote aliyonipangia; na mengi kama hayo yako katika akili yake. Kwa hivyo, ninatetemeka kwa hofu mbele yake; hata nikifikiri tu ninapatwa na woga. Mungu amefanya moyo wangu uregee, Mungu Mwenye Uwezo amenitia hofu. Maana nimepatwa na giza, na giza kubwa limetanda katika uso wangu. Mbona Mungu Mwenye Uwezo hapangi wakati wa hukumu? Kwa nini wanaomujua hawajui hizo siku zake? Watu wanaondoa vitambulisho vya mipaka ya mashamba, na wengine wanaiba makundi ya nyama na kuwafuga. Wananyanganya wayatima punda wao, wanatwaa ngombe dume wa mujane kuwa rehani. Wanasukuma wamasikini kandokando ya barabara; wamasikini wa dunia wanajificha mbele yao. Kwa hiyo kama punda wa pori katika jangwa, wanatoka mapema kwenda kutumika, wakitafuta chakula kwa bidii, kusudi wapate chochote cha kukulisha watoto wao. Wamasikini wanalazimishwa kuvuna mashamba ya wengine, wanaokota katika shamba la mizabibu la waovu. Usiku kucha wanalala uchi bila nguo, wakati wa baridi hawana cha kujifunikia. Wanalowana kwa mvua ya juu ya milima, wanajibanisha kwenye mawe kwa ukosefu wa makimbilio. Kuna watu wanaoondoa watoto wayatima kwenye vifua vya mama yao. Wengine wanatwaa nguo ya masikini kuwa rehani. Wamasikini wanatembea uchi, bila nguo; wenye njaa wanabeba miganda ya ngano. Wanawatengenezea waovu mafuta yao, au kukamua divai bila hata kuionja. Kutoka katika muji, kilio cha wanaokufa kinasikilika, na walioumizwa wanalalamika kuomba musaada. Lakini Mungu hasikilizi kabisa maombi yao. Kuna wengine waovu wasiopenda mwangaza, wasiofahamu njia za mwangaza, na hawapendi kushika njia zake. Mwuaji anaamuka asubui mapema, kwa kwenda kuwaua wamasikini na wakosefu, na usiku ukifika, kazi yake ni kuiba. Muzinzi naye anangojea giza liingie, akisema: “Hakuna atakayeniona”; kisha anaficha uso wake kwa nguo. Usiku wezi wanavunja nyumba, lakini muchana wanajifungia ndani; wala hawajui kabisa mwangaza ni nini. Kwao wote giza kubwa ni mwangaza wa asubui; wao ni warafiki za vitisho vya giza kubwa. Lakini munasema: “Waovu wanapelekwa haraka na mafuriko ya maji, makao yao yanabaki kuwa inchi iliyolaaniwa; hakuna anayeenda kwenye mashamba yao ya mizabibu.” Kama vile teluji inavyoyeyuka katika joto na kipwa ndivyo kuzimu inavyotowesha waovu. Maana muzazi wao anawasahau watu hao, hakuna atakayewakumbuka tena. Ndivyo uovu ulivyovunjika kama muti. Waovu wanatesa wanawake wasiopata watoto wala hawawatendei vizuri wanawake wajane. Mungu, kwa nguvu yake, anawaangamiza wenye uwezo; anasimama, nao wanakata tamaa ya kuishi. Anawaacha waovu wajione salama, lakini macho yake yanachunguza mienendo yao. Waovu wanafanikiwa kwa muda tu, kisha wanatoweka, wananyauka na kufifia kama vile jani, wanakatwa kama vile masuke ya ngano. Nani basi, anayeweza kuhakikisha kwamba mimi ni mwongo na kuonyesha kwamba maneno yangu si kweli? Kisha Bildadi wa inchi ya Suhi akajibu: Mungu ni mwenye uwezo mukubwa, watu wote wamwogope. Yeye anaweka amani mpaka juu kwake mbinguni. Nani anayeweza kuhesabu majeshi yake? Ni nani asiyeangaziwa na mwangaza wake? Mutu anaweza basi namna gani kuwa mwenye haki mbele ya Mungu? Mwanadamu tu anaweza namna gani kujidai kuwa safi? Kwake Mungu, hata mwezi hauangai vya kutosha, nyota nazo si safi mbele yake; ni nini sasa mutu ambaye ni kidudu, mwanadamu ambaye ni nondo tu! Kisha Yobu akajibu: Aa! Jinsi gani ulivyomusaidia asiyekuwa na uwezo! Jinsi gani ulivyomwokoa asiyekuwa na nguvu! Jinsi gani ulivyomushauri asiyekuwa na hekima, na kumushirikisha ujuzi wako! Lakini umesema hayo kwa ajili ya nani? Nani aliyekusukuma kuongea hivyo? Mizimu kule chini inatetemeka, maji ya chini na wakaaji wake yanaogopa. Kuzimu kuko wazi kabisa mbele ya Mungu. Shimo la kuangamia halina kifuniko chochote. Mungu anatandaza kaskazini juu ya pahali patupu, na anatundika dunia pahali pasipo kuwa kitu. Anayafunga maji katika mawingu yakuwe mazito, nayo mawingu hayapasuki kwa uzito wake. Anaufunika uso wa mwezi na kutandaza juu yake wingu. Amechora muviringo juu ya uso wa bahari, penye mpaka kati ya mwangaza na giza. Mungu akitoa sauti ya kukaripa, nguzo za mbingu zinatetemeka na kushangaa. Kwa nguvu zake alituliza bahari; kwa maarifa yake alimwangamiza Rahabu. Kwa pumzi yake alisafisha anga; mukono wake ulitoboa nyoka mukubwa anayeruka. Ikiwa haya ni machache tu ya matendo yake, ni minongono tu tunayosikia juu yake, nani anayeweza kujua ukubwa wa nguvu yake? Yobu akaendelea kutoa masemi yake, akasema: Kama vile Mungu anavyoishi, aliyeniondolea haki yangu, Mungu Mwenye Uwezo aliyeifanya nafsi yangu ikuwe na uchungu, ninaapa kwamba kadiri ninavyoweza kupumua, roho ya Mungu ikiwa bado ndani yangu, midomo yangu haitasema uongo hata kidogo, wala ulimi wangu kusema udanganyifu. Siwezi kabisa kusema kwamba ninyi munasema ukweli. Mpaka kufa kwangu ninasema sina kosa. Ninashikilia haki yangu, wala sitaiacha; katika zamiri yangu sina cha kunihukumu katika maisha yangu. Adui yangu apate azabu ya mwovu, anayesimama kunishambulia aazibiwe kama mubaya. Asiyemwogopa Mungu ana tumaini gani wakati Mungu anapokata pumzi yake, anapomwondolea uzima wake? Wakati atakapopatwa na taabu, Mungu atasikia kilio chake? Mwovu hawezi kufurahi mbele ya Mungu Mwenye Uwezo; hataweza kudumu akimwomba Mungu. Nitawafundisha jinsi kitendo cha Mungu kinavyokuwa, sitawaficha mipango ya Mungu Mwenye Uwezo. Lakini ninyi munajua jambo lile vizuri sana! Mbona, basi munasema maneno yasiyokuwa na maana? Hiki ndicho Mungu alichomwekea mutu mwovu; mutesaji alichopangiwa kupata ni hiki: Watoto wake hata wakuwe wengi watauawa kwa upanga; wazao wake hawatakuwa na chakula cha kutosha. Wale watakaopona watakufa kwa ugonjwa mukali, na wajane wao hawatawaomboleza. Hata akilundika feza kama vile mavumbi, na nguo kama vile udongo wa mufinyanzi, yeye alundike tu, lakini mwenye haki ndiye atakayezivaa, na feza yake watu wasiokuwa na kosa wataigawanyana. Nyumba mwovu anayojenga ni kama vile utando wa buibui, ni kama vile kibanda cha mulinzi katika shamba. Anakwenda kulala akiwa tajiri, lakini ni mara ya mwisho; atafungua macho yake, na utajiri wake umetoweka! Vitisho vinamufikia kama vile mafuriko; usiku anapatwa na zoruba. Upepo mukali wa mashariki unamupeperusha naye anatoweka; unamufagilia mbali kutoka makao yake. Upepo ule unamufunika bila huruma; anajaribu kukimbia lakini mbio za bure. Upepo unamupigia vigelegele anapokimbia, na kumuzomea toka pahali pake. Hakika kuna nafasi ya kuchimba feza, na pahali ambako zahabu inasafishwa. Watu wanachimba chuma ndani ya udongo, wanayeyusha shaba kutoka mawe ya madini. Wachimba madini wanaleta taa katika giza, wanatafutatafuta mpaka chini zaidi ya udongo, na kuchimbua mawe yenye madini katika giza. Mwanadamu anachimba mashimo mbali na makao ya watu, mbali na watu pahali kusipofikiwa, wachimba madini wananinginia wakifungwa kamba. Kutoka ndani ya udongo chakula kinapatikana, lakini chini yake kila kitu kinavurugwa kwa moto. Katika mawe yake kunatoka mawe ya yakuti, na udongo wake una mavumbi ya zahabu. Njia ya kwenda kule hakuna ndege mukula nyama anayeijua; na wala jicho la tai halijaiona. Nyama wakali hawajaikanyaga wala simba mwenyewe hajapita ndani yake. Mwanadamu anachimbua mawe magumu kabisa, anachimbua milima mpaka kwenye misingi yake. Anapasua mifereji kati ya mawe makubwa, na jicho lake linaona mawe ya bei kali. Anaziba chemichemi zisitiririke, na kufichua vitu vilivyofichwa. Lakini hekima itapatikana wapi? Ni pahali gani panapopatikana maarifa? Hakuna mutu anayejua bei ya hekima, wala hekima haipatikani katika inchi ya wanaokuwa wazima. Vilindi vinasema: “Hekima haiko kwetu.” Bahari inasema: “Haiko kwangu.” Hekima haiwezi kupatikana kwa zahabu, wala kwa kupima kiasi kingi cha feza. Haiwezi kupimwa kwa zahabu ya Ofiri, wala kwa mawe ya sardoniki au ya yakuti samawi. Zahabu au kioo havilingani nayo, wala haiwezi kubadilishwa na mawe ya zahabu safi. Hekima ina bei kali kuliko mawe ya matumbawe na marijani, bei kali yake inashinda bei kali ya ushanga. Topazi ya Etiopia haiwezi kulinganishwa nayo, wala haiwezi kupewa bei ya zahabu safi. Basi, hekima inatoka wapi? Ni wapi panapopatikana maarifa? Imefichwa mbali na macho ya viumbe vyote vyenye uzima, na ndege hawawezi kuiona. Shimo la kuangamia na Kifo wanasema: “Tumesikia uvumi wake kwa masikio yetu.” Mungu anajua njia ya hekima, anajua pahali inapopatikana. Maana yeye anaona mpaka kwenye miisho ya dunia, anaona kila kitu chini ya mbingu. Alipoupa upepo uzito wake na kuyapimia maji mipaka yake, alipoamua mvua inyeshe wapi, umeme na radi vipite wapi, pale ndipo alipoiona hekima na kuitangaza. Aliisimika na kuichunguza. Kisha Mungu akamwambia mwanadamu: Sikia! Kumwogopa Bwana ndiyo hekima, na kujitenga na uovu ndiyo maarifa. Kisha Yobu akaendelea na masemi yake, akasema: Heri ningekuwa kama zamani, wakati ule ambapo Mungu alinichunga, wakati taa yake iliponiangazia juu ya kichwa, na kwa mwangaza wake nilitembea katika giza. Wakati ule nilifikia ukamilifu wa maisha, wakati urafiki wa Mungu ulikaa ndani ya nyumba yangu. Mungu Mwenye Uwezo alikuwa angali pamoja nami, na watoto wangu walinizunguka. Nyakati hizo niliogelea kwenye fanaka. Mawe yalinitiririshia vijito vya mafuta. Nilipokutana na wazee kwenye mulango wa muji na kutwaa nafasi yangu katika mukutano, vijana waliponiona walisimama pembeni, na wazee walisimama wima kwa heshima. Wakubwa waliponiona waliacha kuzungumuza, waliweka kidole juu ya midomo kuwaomba watu wakae kimya. Sauti za waheshimiwa zilinyamazishwa, na vinywa vyao vikafumbwa. Kila mutu aliyesikia habari zangu alinitakia heri na aliponiona, alikubali habari zile kuwa kweli. Nilimwokoa masikini aliyenililia kupata musaada, vilevile na yatima asiyekuwa na wa kumusaidia. Waliokuwa karibu kuangamia walinitakia baraka. Niliwafanya wajane waone tena furaha ndani ya moyo. Haki ilikuwa ndiyo nguo yangu; kufuata sheria ya Mungu kulikuwa kama vile kanzu na taji langu. Kwa vipofu nilikuwa macho ya kuwaonyesha njia; kwa viwete nilikuwa miguu yao. Kwa wamasikini nilikuwa baba yao; nilifanya bidii kutetea haki za watu nisiowajua. Nilivunja nguvu za watu waovu, nikawafanya wawaachilie mateka wao. Kisha nikafikiri: “Nitakufia ndani ya chicha yangu,” na siku za maisha yangu zitaongezeka kama vile muchanga. Mimi ni kama vile muti uliotandaza mizizi ndani ya maji; umande wa usiku unanyesha juu ya matawi yangu. Ninapata utukufu mupya siku zote, na nguvu zangu tayari kama vile mushale na upinde. Wakati ule watu walinisikiliza na kungoja, walikaa kimya kungojea mashauri yangu. Nilipomaliza kusema hawakukuwa na cha kuongeza; maneno yangu yaliwakolea kama vile matone ya mvua. Watu waliningojea kama vile wanavyongojea mvua, walikuwa kama vile watu wanaotazamia mvua ya kwanza. Walipokata tamaa, niliwaonyesha uso wa furaha; walishika muchangamuko wa uso wangu. Niliwatangulia kwa kuwaongoza, nikawaonyesha njia. Nilikuwa kwao kama vile mufalme kati ya majeshi yake; kama vile mutu anayewafariji wenye musiba. Lakini sasa watu wananichekelea, tena watu wanaokuwa wadogo kuliko mimi; watu ambao niliwaona baba zao hawafai hata kuwahesabu kama imbwa wangu wakilinda kondoo. Ningepata faida gani katika mikono yao, watu ambao nguvu zao zilikuwa zimewaishia? Katika ukosefu na njaa kali walitafutatafuta kitu cha kutafuna katika jangwa, sehemu tupu zisizokuwa na chakula. Walichuma mimea katika jangwa na majani katika pori wakakula, walikula hata mizizi ya muti wa vifagio. Walifukuzwa mbali na watu, watu waliwapigia kelele kama wezi. Iliwapasa kutafuta usalama katika mifereji kwenye maporomoko, katika mashimo ndani ya udongo na mawe. Kule katika vichaka walilia kama nyama, walikusanyika pamoja chini ya nyasi. Walikuwa wapumbafu wakubwa na waovu ambao walilazimishwa kufukuzwa katika inchi kwa fimbo. Na sasa wamenitungia wimbo wa kunizomea, nimekuwa kitu cha kuchekesha kwao. Wananichukia na kuniepuka; wakiniona tu wanatema mate kwenye uso. Kwa maana Mungu ameniregeza na kunishusha, wamekuwa huru kunitendea wanavyopenda. Kundi la watu linasimama kwa kunishitaki, likitafuta kuniangusha kwa kunitegea. Linanishambulia kusudi niangamie. Watu hao wanakata njia yangu, wanazidisha hasara yangu, na hakuna mutu wa kuwazuia. Wanakuja kama kwenye njia kubwa, na kisha mashambulio wanasonga mbele. Hofu kubwa imenishika. Heshima yangu imetoweka kama kwa upepo, na raha yangu imepita kama wingu. Sasa sina nguvu yoyote ndani ya nafsi yangu; siku za mateso zimenipata. Usiku mifupa yangu yote inauma; maumivu yanayonitafuna hayapoi. Mungu amenishika kwa nguo zangu, amenibana kama shingo ya kanzu yangu. Amenitupa katika matope; nimekuwa kama majivu na mavumbi. Ninakulilia, lakini haunijibu, ninasimama kuomba lakini haunisikilizi. Umegeuka kuwa mukali kwangu, unanitesa kwa mukono wako wenye nguvu. Unanitupa katika upepo na kunipeperusha; unanitupatupa huku na kule katika zoruba kali. Kweli! Ninajua utanipeleka tu katika kifo, pahali wote wanaoishi watakapokutana. Basi, mutu akiangamia hainui mukono? Mutu akiwa tabani haombi musaada? Sikuwalilia wale waliokuwa na taabu? Sikuona uchungu kwa ajili ya wamasikini? Lakini nilipotazamia mazuri, mabaya yalinipata; nilipongojea mwangaza, giza lilikuja. Moyo wangu unahangaika wala hautulii hata kidogo. Siku za mateso zimenipata. Ninapitapita nikiomboleza. Kwangu hakuna jua. Ninasimama katika makutano kuomba musaada. Kwa kilio nimekuwa ndugu ya imbwa wa pori, kati ya mimi na mbuni hakuna tofauti. Ngozi yangu inakuwa nyeusi na inachubuka, mifupa yangu inaungua kwa homa. Kinubi changu kimekuwa cha kufanya kilio filimbi yangu kwa ajili ya kuomboleza. Nimejizuiza kabisa mimi mwenyewe, macho yangu yasimwangalie binti kwa tamaa. Au, ninangojea nini kutoka kwa Mungu anayekuwa juu? Mungu Mwenye Uwezo ameniwekea kitu gani? Hasara haipati watu waovu na maangamizi wale wanaotenda mabaya? Mungu haoni njia zangu na kujua hatua zangu zote? kama hatua zangu zimepotoka nao moyo wangu ukafuata tamaa za macho yangu, kama mikono yangu imechafuliwa na zambi, basi nipande na mwingine akule, mazao yangu ya shamba yaongolewe. Kama moyo wangu umevutwa kwa muke wa mutu, kama nimevizia kwenye mulango wa jirani yangu, basi, muke wangu amupikie mume mwingine, na wanaume wengine walale naye. Jambo hilo ni kosa la kuchukiza, uovu ambao mwamuzi anapaswa kuazibu. Kosa langu lingekuwa kama vile moto wa kuniteketeza na kuangamiza, na kuchoma kabisa mapato yangu yote. Kama nimekataa maneno ya mutumishi au mujakazi wangu, waliponiletea malalamiko yao, nitafanya nini basi Mungu atakaposimama mbele yangu? Akinichunguza, nitamujibu nini? Maana Mungu ndiye aliyeniumba mimi na mutumishi wangu; yeye ndiye aliyetuumba sisi wote. Nimepata kumukatalia masikini mahitaji yake au kuwafanya wajane watumaini bure? Nimekula chakula changu peke yangu, bila kuwaachia wayatima nao wapate kitu chochote? Hapana! Tangu ujana wangu nimekuwa baba yao aliyewalea, tangu utoto wangu nimewaongoza wajane. Nilipoona mutu anakufa kwa kukosa nguo, au masikini ambaye hana nguo ya kuvaa, nilimupa joto kwa nguo za manyoya ya kondoo wangu naye akanitakia baraka za shukrani ya moyo. Kama nimekunjia yatima ngumi katika tribinali nikijua nitapendelewa na waamuzi, basi, bega langu liongoke, mukono wangu ukwanyuke kwenye maungio yake. Maana hasara kutoka kwa Mungu ni kitisho kwangu; mimi siwezi kusimama mbele ya ukubwa wake. Sikuweka tumaini langu katika zahabu, sikuiambia zahabu safi: “Wewe ni usalama wangu”, sikupata kufurahia wingi wa utajiri wangu au kujivunia mapato mengi ya mikono yangu. Sikuangalia jua likiangaza au mwezi ukipita katika uzuri wake kusudi niviabudu kwa siri, na kubusu mikono yangu kwa heshima yake. Huo ungekuwa uovu wa kuazibiwa na waamuzi maana ningekuwa mwongo mbele ya Mungu anayekuwa juu. Nimefurahia kuangamia kwa adui yangu, au kufurahi alipopatwa na hasara? Hapana! Sikuruhusu kinywa changu kusema mabaya juu yake, kwa kumulaani kusudi akufe. Watumishi wangu wote wanasema wazi, kila mugeni amekaribishwa katika nyumba yangu. Musafiri hakulala inje ya nyumba yangu; nilimufungulia mulango mupita njia. Nimeficha makosa yangu kama wengine? Nimekataa kutambua zambi zangu? Sijaogopa kusimama mbele ya kundi la watu wala kukaa kimya au kujifungia ndani, kwa kuogopa kutishwa na mazarau yao. Heri kungekuwa mutu wa kunisikiliza! Ninaweza kutia sahihi yangu katika kila neno nililosema. Mungu Mwenye Uwezo anijibu! Heri mashitaki waadui zangu wanayonitolea yangeandikwa! Ningeyabeba kwa sifa juu ya mabega yangu na kuyavaa kwenye kichwa kama taji. Ningemuhesabilia Mungu kila kitu nilichofanya, ningemwendea kama mwana wa mufalme. Kama nimeiba shamba ninalolima na kusababisha mifereji yake iomboleze, kwa kufaidika na mazao yake bila kulipa na kusababisha kifo cha wenyeji, basi miiba iote mule pahali pa ngano, na magugu pahali pa shayiri. Mwisho wa masemi ya Yobu. Basi hawa watu watatu: Elifasi, Bildadi na Zofari, wakaacha kumujibu Yobu kwa vile alijiona kuwa mwenye haki. Kwa hiyo Elihu mwana wa Barakeli wa kabila la Buzi wa ukoo wa Rama akakasirika. Alimukasirikia Yobu kwa sababu Yobu alijiona yeye mwenye haki na wala si Mungu. Vilevile, aliwakasirikia warafiki watatu wa Yobu kwa sababu hawakukuwa na neno la kumujibu Yobu, na kwa hiyo wakaonyesha kwamba Mungu amekosa. Elihu alikuwa amekaa kimya wakati wale wazee waliposema na Yobu kwa maana yeye alikuwa kijana kuliko wao. Lakini alipoona wale watu watatu wameshindwa kumujibu Yobu, akawaka hasira. Basi, Elihu mwana wa Barakeli wa kabila la Buzi, akaanza kusema: Mimi ni kijana, ninyi ni wazee zaidi. Kwa hiyo niliogopa kuwaambia mawazo yangu. Nilisema ndani ya moyo: “Uwaache wenye siku nyingi waseme, wenye miaka mingi wafundishe hekima.” Lakini ile roho inayokuwa ndani ya mutu, ile pumzi ya Mungu Mwenye Uwezo, ndiyo inayomwezesha mwanadamu kufahamu. Si lazima kuwa muzee kusudi ukuwe na hekima; haiko wazee tu ndio wenye kufahamu jambo linalokuwa sawa. Kwa hiyo ninasema: “Munisikilize, muache nami nitoe maoni yangu.” Basi, mimi nilingojea kile mulichotaka kusema, nilisikiliza misemo yenu ya hekima, mulipokuwa munajaribu kutafuta neno la kusema. Niliwasikiliza kwa uangalifu sana, lakini hakuna hata mumoja wenu aliyemushinda Yobu; wote mulishindwa kujibu kwa maneno yake. Kwa hiyo musiseme: “Sasa tumepata hekima. Atakayemushinda ni Mungu, wala si mwanadamu.” Maneno ya Yobu hayakukuwa kwa ajili yangu. Kwa hiyo sitamujibu kama vile mulivyomujibu ninyi. Ninyi mumeshangaa na kukaa kimya; ninyi hamuna cha kusema zaidi. Basi, ningoje tu kwa vile hamusemi, kwa sababu munakaa tu bila kujibu kitu? Mimi vilevile nitatoa jibu langu; mimi nitatoa vilevile maoni yangu. Niko na maneno mengi sana, roho yangu inanisukuma kusema. Moyo wangu umefurika kama divai iliyozibwa, kama kibuyu cha divai mupya tayari kupasuka. Ni lazima niseme kusudi nipate kutulia; inanipasa kufungua kinywa changu na kujibu. Sitamupendelea mutu yeyote wala kutumia maneno ya kubembeleza mutu, maana mimi sijui kubembeleza mutu. Kama si vile, Muumba wangu angeniangamiza. Sasa, Yobu, sikiliza masemi yangu; sikiliza maneno yangu yote. Sikia! Ninafumbua kinywa changu. Ulimi wangu utasema. Nitasema kadiri ya usawa wa moyo wangu; ninayoyajua nitayasema kwa uaminifu. Roho ya Mungu iliniumba, nayo pumzi ya Mungu Mwenye Uwezo inanipa uzima. Unijibu, kama unaweza. Panga masemi yako vizuri mbele yangu, ushike musimamo wako. Wewe na mimi ni sawa mbele ya Mungu; mimi vilevile niliumbwa kwa sehemu ya udongo. Kwa hiyo hauna sababu ya kuniogopa; maneno yangu mazito hayatakulemea. Kweli umesema, nami nikasikia; nimesikia yote uliyosema. Wewe umesema hivi: “Mimi niko safi, wala sina kosa. Hakuna ubaya wowote katika moyo wangu. Mungu ananitafutia sababu, ananiona kama adui yake. Ananifunga miguu kwa minyororo, na kuchunguza hatua zangu zote.” Lakini Yobu, ninakuambia pale umekosa. Mungu ni mukubwa kuliko mwanadamu. Kwa nini unashindana naye, ukisema hatajibu ulizo lako moja? Mungu anaweza kusema kwa njia moja au ingine lakini mutu hatambui. Mungu anaongea na watu katika ndoto na maono, wakati usingizi muzito unapowapata, wanaposinzia katika vitanda vyao. Halafu anawafungua watu masikio yao; anawatia hofu kwa maonyo yake, wapate kuachana na matendo yao mabaya, na kuvunja kiburi chao. Hivyo anamukinga mutu asiangamie katika shimo, maisha yake yasiangamie kwa upanga. Mungu anamwazibu mutu kwa maumivu yanayomuweka katika kitanda, maumivu yanashika viungo vyake bila kukoma; naye anapoteza hamu yote ya chakula, hata chakula ni chukizo kwake. Mwili wake unakonda hata hawezi kutambuliwa, na mifupa yake iliyofichama ikatokea inje. Yuko karibu sana kuingia ndani ya kaburi, na maisha yake karibu na wale wanaoleta kifo. Lakini inawezekana kwamba malaika, ambaye ni mupatanishi mumoja kati ya maelfu, atakuwa karibu na mutu yule kwa kumufunulia jambo la kufanya. Yule malaika anaweza kumwonea huruma na kumwomba Mungu: “Umwokoe asiingie katika shimo; nimepata ukombozi wake.” Mwili wake utaweza kuwa tena kama kijana, ataweza kurudilia tena nguvu zake za ujana. Kisha atamwomba Mungu na kukubaliwa, atakuja mbele yake kwa furaha, na Mungu atamurudishia utukufu wake. Atashangilia mbele ya watu na kusema: “Nilitenda zambi na kupotosha usawa, nami sikuazibiwa kutokana na hayo. Mungu aliniokoa nisiangamie katika shimo; nimebaki muzima na ninaona mwangaza.” Sikia! Mungu anamufanyia mwanadamu haya yote, tena mara mbili, mara tatu. Anamwokoa mwanadamu asiangamie katika shimo, aweze kuona mwangaza wa maisha. Sikia Yobu, unisikilize kwa uangalifu; ukae kimya, nami nitasema. Kama una la kusema, unijibu; sema, maana ninataka kukuona bila kosa. Kama sivyo, nyamaza unisikilize, ukae kimya nami nikufundishe hekima. Kisha Elihu akaendelea kusema: Musikilize maneno yangu, enyi wenye hekima, munitegee masikio yenu, ninyi wenye ujuzi. Sikio linapima maneno, kama vile ulimi unavyoonja chakula. Basi, tuchague sasa yanayokuwa sawa, tuamue kati yetu yanayokuwa mazuri. Basi, Yobu amesema: “Mimi Yobu sina kosa, Mungu ameniondolea haki yangu. Ingawa sina kosa, ninaonekana kuwa mwongo. Kidonda changu hakiponi ingawa sina kosa.” Ni nani anayekuwa kama Yobu ambaye kwake mazarau ni kama kunywa maji? Anaandamana na watenda maovu, anatembea na watu waovu. Maana amesema: “Mutu hapati faida yoyote na kujisumbua kumupendeza Mungu.” Kwa hiyo munisikilize, enyi wenye ujuzi. Mungu hawezi kufanya uovu hata kidogo; Mungu Mwenye Uwezo hawezi kufanya kosa. Mungu atamulipa mutu kadiri ya matendo yake, atamulipiza kulingana na mwenendo wake. Ni ukweli mutupu: Mungu hafanyi jambo ovu. Mungu Mwenye Uwezo hapotoshi haki hata kidogo. Kuna yule aliyemupatia mamlaka juu ya dunia? Uwezo wake juu ya ulimwengu ni wake peke yake. Kama Mungu angejifikiri tu yeye mwenyewe, akiondoa pumzi yake ya uzima katika dunia, viumbe vyote vingeangamia kabisa, naye mwanadamu angerudi katika mavumbi. Kama una akili sikiliza; sikiliza ninachokuambia. Anayetawala ulimwengu kwa sheria zake anachukia haki? Utasubutu kumuhukumu mwenye haki na mwenye nguvu, anayemwambia mufalme “Wewe ni wa ovyo!” na watu wenye heshima “Ninyi ni waovu!” Yeye hawapendelei wakubwa, wala kuwajali watajiri kuliko wamasikini, maana wote hao ni kazi ya mikono yake. Kufumba na kufumbua hao wamekufa; wanatikiswa usiku na kuaga dunia; nao wenye nguvu wanaondolewa bila kutumia nguvu za mutu. Macho ya Mungu yanachunguza mienendo ya watu; yeye anaziona hatua zao zote. Hakuna weusi wala giza kubwa ambamo watenda maovu wanaweza kujificha. Mungu hahitaji kumujulisha mutu wakati wa kumuleta mbele ya tribinali yake. Anawaangamiza wenye nguvu bila uchunguzi, na kuwaweka wengine pahali pao. Kwa maana anayajua matendo yao yote, anawapindua usiku waangamie. Anawapiga mbele ya watu kwa ajili ya uovu wao, kwa sababu wameacha kumufuata yeye, wakazarau njia zake zote. Hata wakasababisha kilio cha wamasikini kimufikie Mungu. Mungu akasikiliza kilio cha wale walioteswa. Kama Mungu akinyamaza, nani anayeweza kumuhukumu? Kama akificha uso wake, nani anayeweza kumwona, ikiwa ni taifa au mutu mumoja? Anafanya hivyo, mutu mubaya asitawale, au wale wanaohatarisha maisha ya watu. Labda mutu atamwambia Mungu hivi: “Nimekosa, sitatenda zambi tena. Unionyeshe makosa nisiyoweza kuyaona. Kama nimetenda mabaya, sitayarudilia tena.” Mungu atapaswa kumwazibu kama unavyoona wewe? Wewe ndiwe unayeamua, wala si mimi. Basi, sema unachofikiri wewe. Mutu yeyote mwenye akili, na kila mwenye hekima anayenisikiliza atasema: “Yobu anaongea bila kutumia akili, maneno yake hayana maana.” Heri Yobu angechunguzwa mpaka mwisho, kwa maana anajibu kama watu waovu. Anaongeza uasi juu ya zambi zake; anaeneza mashaka kati yetu, na kuzidisha maneno yake juu ya Mungu. Kisha Elihu akaendelea kusema: Yobu, unaona jambo hili ni sawa? Unasema: “Mimi ni mwenye haki mbele ya Mungu.” Tena unauliza: “Nimepata faida gani kama sikutenda zambi? Nimefaidika kuliko kama vile ningetenda zambi?” Mimi nitakujibu wewe na warafiki zako vilevile. Basi uangalie mbingu! Angalia mawingu yanayokuwa juu kuliko wewe! Ukitenda zambi, Mungu ndiye unayemuzuru? Na kama ukizidisha makosa yako, unazani unamwumiza? Kama wewe ni mwenye haki, unamupatia faida, au yeye anapokea kitu kutoka kwako? Uovu wako utamuzuru mwanadamu kama wewe, haki yako itamufalia mwanadamu mwenzako. Kwa sababu ya mateso mengi watu wanalia, wanaomba musaada kwa sababu ya mapigo ya wenye nguvu. Lakini hakuna anayesema: “Yuko wapi Mungu, Muumba wangu, mwenye kunifanya nichangamuke usiku, anayetuelimisha kuliko nyama, na kutufanya wenye hekima kuliko ndege!” Watu wale wanaomba musaada lakini Mungu hawajibu, kwa sababu ya majivuno ya watu waovu. Kweli Mungu hasikilizi kilio cha bure; Mungu Mwenye Uwezo hajali kilio kile. Atakujibu namna gani wakati wewe unasema kwamba haumwoni na kwamba maneno yako iko mbele yake na wewe unamungojea! Sasa, kwa vile Mungu anazuia hasira yake, wala hajali sana makosa ya watu, Yobu anafungua kinywa kusema maneno matupu, anazidisha maneno bila akili. Kisha Elihu akaendelea kusema: Univumilie kidogo, nami nitakuonyesha kitu; maana ningali bado na cha kusema kwa ajili ya Mungu. Nitaleta hekima yangu kutoka mbali sana, na kuonyesha kwamba Muumba wangu ni wa haki. Kweli maneno yangu si ya uongo; mwenye elimu kamili yuko hapa nawe. Sikia! Mungu ni mwenye nguvu wala hamuzarau mutu yeyote; uwezo wa akili yake ni mukubwa sana! Hawaachilii waovu waendelee kuishi; lakini anawapatia wanaoteswa haki zao. Haachi kuwalinda watu wa haki; nao anawaweka kuwa wafalme watawale na kutukuzwa. Lakini kama watu wakifungwa minyororo, wakinaswa katika kamba za mateso, Mungu anawaonyesha matendo yao maovu, na kwamba wao ni watu wenye kiburi. Anafungua masikio wasikie mafundisho, na kuwaamuru warudi na kuacha uovu. Wakimutii Mungu na kumutumikia, wanafanikiwa katika siku zao zote; miaka yao yote inakuwa ya furaha. Lakini wasipomutii, wanaangamia kwa upanga, na kufa kwa kukosa akili. Waovu wanapenda kukasirika; hawamwombi musaada anapowafunga. Wanakufa wangali bado vijana, maisha yao yanaisha kama ya washerati. Lakini Mungu anawaokoa wenye kuteswa kwa mateso yao, anatumia shida zao kwa kuwafumbua macho. Mungu alikutoa katika taabu, akakuweka pahali pakubwa pasipo shida, na juu ya meza yako amekutayarishia vyakula vizuri. Lakini sasa umehukumiwa kama mwovu, hukumu ya haki imekupata. Angalia kasirani isikuvute kwa kuzarau, au usiache ukubwa wa mali za kukukomboa ukupotoshe. Kilio chako kitafaa kukutoa katika taabu, au nguvu zako zote zitakusaidia? Usitamani usiku ukuje, ambapo watu wanapotoweka. Angalisho! Usielekee uovu maana umepewa mateso kwa kukuepusha na uovu. Kumbuka ukubwa wa uwezo wa Mungu; nani anayeweza kufundisha kama yeye? Nani basi aliyeweza kumupangia njia yake, au anayeweza kumwambia: “Umekosa”? Usisahau kusifu matendo yake ambayo watu wameyashangilia. Watu wote wameona mambo Mungu aliyofanya; mwanadamu anayaona kutoka mbali. Mungu ni mukubwa sana hata hatuwezi kumujua; muda wa maisha yake hauchunguziki. Yeye anayavuta kwake maji ya bahari, na kutoka ukungu anafanya matone ya mvua. Anayafanya mawingu yanyeshe mvua, na kuwatiririshia wanadamu kwa wingi. Nani anayejua jinsi mawingu yanavyotanda, au jinsi radi inavyonguruma kwake katika anga? Yeye anatandaza umeme wake kumuzunguka, na kuvifunika vilindi vya bahari. Kwa mvua anawakulisha watu na kuwapatia chakula kwa wingi. Anaukamata umeme kwa mikono yake, kisha anapiga nao shabaha. Radi inatangaza kuja kwa Mungu; hata nyama wanajua kwamba anakuja. Kutokana na hayo, moyo wangu unatetemeka, na kuruka kutoka pahali pake. Musikilize ngurumo ya sauti ya Mungu, na muvumo wa sauti kutoka ndani ya kinywa chake. Anafanya uenee chini ya mbingu yote, anaeneza umeme wake katika pembe zote za dunia. Halafu sauti yake inanguruma, sauti ya Mungu inanguruma kwa utukufu; yeye hazuizi umeme wakati inaposikilika. Mungu anapiga radi ya ajabu kwa sauti yake, anafanya mambo makubwa tusiyoweza kuyaelewa. Anaiambia teluji: “Anguka juu ya inchi!” na manyunyu na mvua: “Nyesha kwa nguvu.” Anafunga shuguli za kila mutu kusudi watu wote watambue kazi yake. Nyama wa pori wanarudi katika maficho yao na kubaki katika mapango yao. Zoruba inavuma kutoka chumba chake, na baridi kali kutoka katika gala yake. Kwa pumzi ya Mungu barafu inatokea, uso wa maji unaganda kwa haraka. Mungu analijaza wingu manyunyu mazito; mawingu yanasambaza umeme wake. Kwa amri yake vyote vinazunguka huku na kule, kutimiza kila kitu anachoviamuru, kufanya katika ulimwengu wa viumbe. Mungu anatimiza mapenzi yake katika dunia, ikuwe ni kwa ajili ya kuwaazibu watu, au kwa ajili ya kuonyesha wema wake. Unapaswa kusikiliza Yobu! Nyamaza, usikilize maajabu ya Mungu. Unajua jinsi Mungu anavyovipa amri yake, na kuyafanya umeme wa mawingu yake uangae? Unajua jinsi mawingu yanavyoelea katika anga? Ndizo kazi za ajabu za yule anayekuwa mukamilifu wa maarifa! Wewe unajiona umevaa nguo za joto sana, wakati upepo wa kusini unapovuma juu ya inchi. Unaweza kuzitandaza mbingu kama yeye hata zikuwe ngumu kama kioo cha shaba? Utufundishe tutakachomwambia Mungu; maana masemi yetu si wazi, tuko katika giza. Yeye anahitaji kujulishwa kwamba ninataka kusema? Au mutu anaweza kujitakia kuangamizwa? Kwa rafla mutu hawezi tena kuona waziwazi: Jua limefichwa nyuma ya mawingu, na upepo umesafisha anga! Mwangaza muzuri unatokea upande wa kaskazini; Mungu amezungukwa na utukufu wa kutisha. Mungu Mwenye Uwezo asiyeweza kufikiwa na mutu, uwezo na haki yake ni mukubwa. Amejaa haki wala hapotoshi sheria hata kidogo. Kwa hiyo, watu wote wanamwogopa. Yeye hawajali watu wanaojiona kuwa wenye hekima. Halafu Yawe akamujibu Yobu kutoka katika zoruba: Nani wewe unayevuruga mipango yangu kwa maneno yasiyokuwa na akili? Ujikaze kama mwanaume, nami nitakuuliza nawe utanijibu. Ulikuwa wapi nilipoiweka misingi ya dunia? Uniambie, kama una maarifa. Ni nani aliyeweka vipimo vyake, unajua bila shaka! Au nani aliyenyoosha kamba juu yake kwa kuipima? Nguzo za dunia zimesimikwa juu ya nini, au nani aliyeliweka jiwe lake la musingi, nyota za asubui zilipokuwa zikiimba pamoja, na wana wa Mungu wakapiga vigelegele vya shangwe? Ni nani aliyefunga mafuriko ya bahari wakati yalipozuka na kuvuma kutoka katika vilindi? Ni nani aliyefunika bahari kwa mawingu na kuiviringishia giza kubwa, aliyeiwekea bahari mipaka na kuizuia kwa vifungio na milango na kuiambia: “Mwisho wako ni hapa, si zaidi! Mawimbi yako ya nguvu yatakomea hapa!” Yobu, tangu uzaliwe umekwisha kuamuru kupambazuke na kufanya mapambazuko yajue pahali pake, kusudi yapate kukamata dunia kwa pembe zake na kuwatikisa watenda mabaya? Dunia inageuka na kupata rangi kama nguo; kama udongo wa mufinyanzi unavyogeuzwa na muhuri. Lakini waovu watanyimwa mwangaza wao, mukono wanaonyoosha kwa kupiga watu utavunjwa. Umepata kufika kwenye chemichemi za bahari au kutembea juu ya sakafu ya kilindi cha bahari? Umekwisha kuonyeshwa milango ya kifo au kuona milango ya makao ya giza kubwa? Unajua ukubwa wa dunia? Uniambie kama unajua haya yote. Makao ya mwangaza yako wapi? Kwenye nyumba ya giza ni wapi, kusudi upate kupeleka kwenye makao yake, na kuifahamu njia ya kwenda kule kwake. Wewe unapaswa kujua, wewe ambaye umekwisha ishi miaka mingi! Umekwisha kuingia katika akiba za teluji, au kuona akiba za mvua ya mawe ambavyo nimeviweka kwa ajili ya wakati wa fujo, kwa ajili ya siku ya mapigano na vita? Unajua mwangaza unagawanywa kwa njia gani, au namna gani upepo wa mashariki unavyosambazwa katika dunia? Nani aliyechora katika anga njia kwa ajili ya mvua? Nani aliyeonyesha radi njia yake katika mawingu, nayo ikasababisha mvua kunyesha katika inchi kusikoishi mutu na katika jangwa ambako hakuna mutu, kusudi ikunyweshe inchi kavu na yenye kukauka na kuifanya ioteshe majani? Mvua ina baba? Au nani amezaa matone ya umande? Barafu ilitoka katika tumbo la nani? Nani aliyezaa teluji? Maji yanageuka kuwa magumu kama jiwe, na uso wa bahari unaganda. Angalia makundi ya nyota: Unaweza kuifunga minyororo Kilimia, au kuviregeza vifungo vya Orioni? Unaweza kuongoza nyota kwa wakati wake, au kumwongoza Dubu pamoja na vitoto vyake? Unayajua maagizo ya mbingu? Unaweza kuzipangia utaratibu wao katika dunia? Unaweza kupiga vigelegele na kuyaamuru mawingu yakufunike kwa mutiririko wa mvua? Wewe ukiamuru umeme uangaze, utakufikia na kusema: “Nipo hapa”? Ni nani aliyemujulisha kwarara kujaa kwa muto Nili au aliyemwambia jogoo kwamba mvua inakuja? Nani mwenye akili ya kuweza kuhesabu mawingu au kuinamisha vibuyu vya maji kule katika mbingu kusudi mavumbi katika dunia yagandamane na udongo ushikamane na kuwa matope? Unaweza kumwindia simba dike au kuishibisha hamu ya simba wakali wanapojificha ndani ya matundu yao, au kulala katika maficho wakivizia? Ni nani anayewapa vibombobombo chakula chao, vitoto vyao vinaponililia mimi Mungu, na kurukaruka huku na kule kwa njaa? Unajua mbuzi wa milima anazaa wakati gani, au umekwisha kuona kulungu akizaa? Unajua anapata mimba kwa muda gani, au siku yenyewe ya kuzaa unaijua? Wanachutama kwa kuzaa, wanazaa vitoto vyao. Vitoto vyao vinapata nguvu, vinakomaa kulekule katika pori, kisha vinawaacha wamama zao na kwenda zao. Nani aliyemwacha huru punda wa pori? Nani aliyewaacha waende kwa kuwafungua? Mimi niliwapa jangwa likuwe nyumba yao, mbuga zenye chumvi kuwa makao yao. Wanajitenga kabisa na makelele ya miji, hawasikilizi kelele la muchungaji. Wanatembeatembea katika milima kwa kupata malisho, na kutafuta kitu chochote kinachokuwa kibichi. Mbogo atakubali kukutumikia? Atakubali kulala katika zizi lako? Unaweza kumufunga mbogo kamba kwa kulima shamba, au akokote jembe la kulima? Utamutegemea kwa sababu ana nguvu nyingi na kumwacha akufanyie kazi zako nzito? Unamutazamia mbogo akuvunie mavuno yako, na kuleta ngano kwenye nafasi ya kupepetea? Mbuni anapigapiga mabawa yake kwa furaha, lakini hawezi kuruka kama korongo. Mbuni anayaacha mayai yake juu ya udongo kusudi yapate joto ndani ya muchanga; lakini hajui kama yanaweza kukanyagwa, au kuvunjwa na nyama wa pori. Mbuni anatendea vitoto vyake kwa ukali kama vile si vyake, hata kazi yake ikiharibika yeye hana wasiwasi; kwa sababu nilimufanya asahau hekima yake, wala sikumupa sehemu yoyote ya akili. Lakini akianza kukimbia, anamuchekelea hata farasi na mupanda-farasi. Yobu, ni wewe ndiwe uliyewapa farasi nguvu, ukawavalisha kwenye shingo manyoya marefu? Ni wewe unayemufanya farasi aruke kama nzige? Mulio wake wa maringo ni wa ajabu! Anakwaruzakwaruza udongo katika mabonde kwa pupa; anakimbilia kwenye mapigano kwa nguvu zake zote. Farasi anaichekelea hofu, na hatishiki; wala upanga hauwezi kumurudisha nyuma. Silaha wapanda-farasi wanazobeba, zinagongana kwa sauti na kuangaa kwenye jua. Farasi anasonga mbele, akitetemeka kwa hasira; baragumu inapolia, yeye hasimami. Kila mara baragumu inapopigwa, yeye anatoa sauti; anasikia harufu ya vita toka mbali, anasikia mushindo wa majemadari wakitoa amri kwa makelele. Mwewe amejifunza kwako jinsi ya kuruka, na kunyoosha mabawa yake kuelekea upande wa kusini? Tai anapanda juu kwa amri yako, na kuweka chicha yake juu kwenye milima? Tai anafanya makao yake juu ya mawe marefu, na incha kali za mawe makubwa ndizo maficho yake. Kutoka kule anavizia nyama, macho yake yanaiona kutoka mbali. Vitoto vyake vinafyonza damu; pale muzoga unapokuwa ndipo tai anapokuwa. Yawe akaendelea kumwambia Yobu: Wewe mwenye kuchunguza makosa utashindana na Mungu Mwenye Uwezo? Wewe unayebishana nami Mungu, basi ujibu mambo hayo! Kisha Yobu akamujibu Yawe: Mimi sifai kitu. Nitakujibu nini? Ninafunga kinywa changu. Nilisubutu kusema na sitasema tena. Nilisema mengi lakini sitaendelea kusema zaidi. Halafu Yawe akamujibu kutoka katika zoruba: Ujikaze kama mwanaume. Nitakuuliza, nawe utanijibu. Unataka kweli kugeuza hukumu yangu, kuniona nina kosa kusudi wewe usikuwe na kosa? Una nguvu kama mimi Mungu? Unaweza kunguruma kwa sauti kama yangu? Basi, ujionyeshe kuwa na utukufu na ukubwa, ujipambe kwa heshima na mamlaka. Uwamwangie watu hasira yako kubwa; umwangalie kila mwenye kiburi na kumwangusha. Umwangalie kila mwenye kiburi na kumuporomosha, uwakanyage waovu pahali wanapokuwa. Uwazike wote pamoja ndani ya udongo; umufunge kila mumoja kwa kifungo cha kifo. Halafu nitakutambua kwa vile nguvu yako mwenyewe imekupa ushindi. Uangalie yule nyama mukubwa kiboko. Nilimwumba kama nilivyokuumba wewe. Yeye anakula majani kama ngombe, lakini ana nguvu ajabu katika mwili wake, na mishipa ya tumbo lake ni imara. Mukia wake ni wenye nguvu kama mwerezi, mishipa ya mapaja yake imeshonwa pamoja. Mifupa yake ni kama mirija ya shaba, mbavu zake ni kama vipande vya chuma. Yeye ni wa kwanza wa ajabu kati ya viumbe vyangu! Ni mimi Muumba wake ninayeweza kumutawala. Milima ambamo nyama wote wa pori wanamochezea inatoa chakula chake. Anajilaza chini ya vichaka vya miiba, na kujificha kati ya matete ndani ya tingitingi. Vivuli vya vichaka vya miiba vinamufunika na vya miti inayoota pembeni ya vijito. Muto ukifurika haogopi, hatishiki hata muto Yordani ukifurikia katika kinywa. Nani anayeweza kuziba macho yake na kumuteka? Nani anayeweza kumutoboa pua kwa mutego? Unaweza kuvua yule nyama mukubwa Leviatani kwa ndoana, au kuufunga ulimi wake kwa kamba? Unaweza kumutia kamba katika pua lake, au kumutoboa taya kwa kulabu? Unazani atakusihi umwachilie? Atazungumuza nawe kwa upole? Atafanya mapatano nawe, umuchukue kuwa mutumishi wako milele? Utacheza naye kama ndege, au kumufunga kamba acheze na wajakazi wako? Unazani wavuvi watashindania bei yake? Wachuuzi watasubutu kumukata na kugawanyana? Wanaweza kuitoboa ngozi yake kwa mikuki, au kichwa chake kwa chuma cha kuvua samaki? Jaribu tu kumugusa: ukifikiri juu ya vita naye, hautarudilia tena kufanya hivyo. Yeyote anayeona yule nyama mukubwa anakufa moyo na kuzimia. Hakuna mutu yeyote mukali anayesubutu kumushitua. Nani, basi anayeweza kusimama mbele yangu? Nani aliyenipa kitu, kusudi nipate kumurudishia? Chochote kinachokuwa chini ya mbingu ni changu. Sitaacha kukuelezea juu ya viungo vya yule nyama mukubwa au juu ya nguvu zake na umbo lake zuri. Nani anayeweza kuondoa nguo yake ya inje? Nani anayeweza kutoboa nguo ya chuma anayovaa? Nani anayeweza kufungua kinywa chake? Meno yake pande zote ni kitisho! Mugongo wake umefanywa kwa mistari ya ngao iliyoshikamana pamoja kama kwa muhuri. Kila mumoja umeshikamana na mwingine, hata hewa haiwezi kupenya katikati yake. Imeunganishwa pamoja, hata haiwezekani kuitenganisha. Akipiga chafya, mwangaza unatokea, macho yake yanametameta kama jua inapotokea. Katika kinywa chake kunatokea mienge inayowaka, cheche za moto zinaruka inje. Katika pua yake kunafuka moshi, kama vile chungu kinachochemuka, kama vile nyasi inayowaka. Pumzi yake inawakisha makaa; ulimi wa moto unatoka ndani ya kinywa chake. Shingo yake ina nguvu ajabu, nyama yule anapotokea watu wanapatwa na hofu. Mishipa yake imeshikamana pamoja, imara kama chuma wala haitikisiki. Moyo wake ni mugumu kama jiwe, mugumu kama jiwe la kusagia. Anapoinuka, mashujaa wanashikwa na woga, kwa pigo moja wanazimia. Hakuna upanga unaoweza kumuumiza, wala mukuki, mushale au nguo ya chuma. Kwake chuma ni laini kama unyasi, na shaba kama muti uliooza. Mushale hauwezi kumukimbiza; akitupiwa mawe ya mujeledi anayaona kama maganda. Kwake, gongo ni kama kipande cha bua; anacheka akitupiwa mikuki kwa wingi. Tumbo lake ni kama limefunikwa na vigae vikali; anakwaruza na kurarua udongo kama chombo cha kulima. Anatikisatikisa bahari kama maji yanayochemuka, anaifanya itoe pofu kama chupa ya mafuta. Anapopita anaacha nyuma kitambulisho kinachoangaa; pofu nyeupe inaonekana ikielea juu ya bahari. Katika dunia hakuna kinachofanana nayo; hicho ni kiumbe kisichokuwa na hofu. Kinawaona kuwa si kitu wote wenye kiburi; hicho ni mufalme wa nyama wote wakali. Kisha Yobu akamujibu Yawe: Ninajua kwamba unaweza kila kitu, lolote unalokusudia haliwezi kuzuiliwa. Ulisema kwamba nilivuruga mipango yako bila akili. Kweli nilitamka kitu ambacho sikuelewa, mambo ya ajabu sana kwangu ambayo sikukuwa ninayajua. Uliniambia nisikilize nawe utaniambia; kwamba utaniuliza nami nikujibu. Kweli nilikuwa nimesikia habari zako kwa masikio tu, lakini sasa ninakuona kwa macho yangu mwenyewe. Kwa hiyo ninatubu na kujihukumu; ninajinyenyekeza na kuikaa juu ya mavumbi na majivu. Yawe alipomaliza kuongea na Yobu, akamwambia Elifasi wa inchi ya Temani: “Kasirani yangu imewaka juu yako na warafiki zako wawili maana hamukusema ukweli juu yangu kama vile mutumishi wangu Yobu alivyofanya. Kwa hiyo mutwae ngombe dume saba na kondoo dume saba, muende kwa mutumishi wangu Yobu, mutoe nyama wale kuwa sadaka ya kuteketezwa kwa ajili yenu. Naye mutumishi wangu Yobu atawaombea, nami nitaisikiliza maombi yake na kuacha kuwatendea kulingana na upumbafu wenu; maana hamukusema ukweli juu yangu kama mutumishi wangu Yobu alivyofanya.” Basi, Elifasi wa inchi ya Temani, Bildadi wa inchi ya Shua, na Zofari wa inchi ya Namati, wakafanya kama vile Yawe alivyowaambia. Yawe akapokea maombi ya Yobu. Nyuma ya Yobu kuwaombea warafiki zake, Yawe akamurudishia Yobu hali yake ya kwanza. Akamupa mara mbili ya yote aliyokuwa nayo pale mbele. Kisha wandugu zake, wadada zake na warafiki wote waliomufahamu mbele wakamwendea kwake, wakakula chakula pamoja naye. Wakamupa pole na kumufariji kwa ajili ya mateso yote ambayo Yawe alikuwa amemuletea. Kila mumoja wao akamupa Yobu feza na pete ya zahabu. Katika miaka ya Yobu iliyofuata, Yawe alimubariki zaidi kuliko hata alivyokuwa amemubariki pale mbele. Basi Yobu akakuwa na kondoo elfu kumi na ine, ngamia elfu sita, ngombe elfu mbili na punda dike elfu moja. Alikuwa vilevile na watoto wanaume saba na wabinti watatu. Binti yake wa kwanza alimupa jina Yemima, wa pili Kezia, na wa mwisho Kereni-Hapuki. Katika inchi yote hiyo hakukukuwa wanawake waliokuwa wazuri kama vile wabinti wa Yobu. Baba yao akawaachia urizi kama vile alivyowaachia kaka zao. Nyuma ya pale, Yobu aliishi miaka mia moja makumi ine, akawaona vijukuu na vitukuu vyake vyote mpaka kizazi cha ine. Basi, Yobu akakufa akiwa muzee wa miaka mingi. Heri mutu asiyefuata shauri la waovu, asiyeshiriki katika njia ya wenye zambi, wala kukusanyika na wenye kuzarau; lakini anafurahia sheria ya Yawe, na kuifikiri muchana na usiku. Huyo ni kama muti uliopandwa kando ya vijito, unaozaa matunda kwa wakati wake, na majani yake hayanyauki hata kidogo. Anafanikiwa katika yote anayofanya. Lakini waovu si vile hata kidogo. Wao ni kama maganda yanayopeperushwa na upepo. Kwa hiyo watu waovu wataanguka wakati wa hukumu, wenye zambi hawatashiriki katika kusanyiko la watu wa haki. Maana Yawe anashugulikia njia ya watu wa haki; lakini njia ya waovu itaangamia. Kwa nini mataifa yanafanya fujo? Mbona watu wanafanya shauri la bure? Wafalme wa dunia wanajitayarisha, watawala wanashauriana pamoja kumwasi Yawe na muchaguliwa wake. Wanasema: “Tujiondoe katika utawala wao; tutupilie mbali minyororo yao!” Yule anayetawala juu mbinguni anawachekelea na kuwazarau. Kisha, anawakaripia kwa kasirani na kuwatisha kwa hasira, akisema: “Nimemusimika mufalme niliyemuchagua; anatawala Sayuni, mulima wangu mutakatifu!” Mufalme anasema: “Nitatangaza amri ya Yawe. Mungu aliniambia: ‘Wewe ni mwana wangu, mimi leo nimekuwa baba yako. Uniombe nami nitakupa mataifa kuwa urizi wako, na dunia nzima kuwa mali yako. Utawaponda kwa fimbo ya chuma, utawavunja kama chungu cha mufinyanzi!’ ” Sasa, enyi wafalme, mutumie akili; musikilize onyo hili, enyi watawala wa dunia. Zaburi ya Daudi. Inaelekea wakati alipomukimbia mwana wake Abusaloma. Ee Yawe, angalia ginsi waadui zangu wanavyokuwa wengi. Ni wengi sana hao wanaonishambulia. Wengi wanasema juu yangu: “Hautapata musaada wowote kwa Mungu.” Lakini wewe, ee Yawe, unanizunguka kama ngao; kwako ninapata utukufu na ushindi. Ninakulilia kwa sauti, ee Mungu, nawe unanisikiliza kutoka kwenye mulima wako mutakatifu. Ninalala na kupata usingizi, ninaamuka tena, maana wewe ni tegemeo langu. Sitaogopa maelfu ya watu wanaonizunguka kila upande. Ee Yawe, ee Mungu wangu, wewe unayevunja waadui zangu wote mataya, unayeponda waovu meno, simama sasa uniokoe! Yawe ndiwe unayeokoa; uwape baraka watu wako. Kwa mukubwa wa waimbaji: kwa vyombo vyenye nyuzi. Zaburi ya Daudi. Ee Mungu, muteteaji wa haki yangu, unijibu ninapoomba. Nilipokuwa katika shida, wewe ulinisaidia; unionee huruma na kusikia maombi yangu. Ninyi watu, mpaka wakati gani mutachafua jina langu? Mpaka wakati gani mutapendelea mambo ya ovyo na kusema uongo? Mujue kwamba Yawe amejichagulia mutu wake wa haki. Yawe anasikia kila mara ninapomwomba. Mukasirike lakini musitende zambi. Mufikiri katika vitanda vyenu na kunyamaza. Mutoe sadaka zinazokuwa sawa, na kumutumainia Yawe. Wengi wanasema: “Heri tungefanikiwa tena! Ee Yawe, utuangalie kwa wema!” Lakini mimi umenijalia furaha kubwa ndani ya moyo, kuliko ya hao wanaokuwa na divai na ngano kwa wingi. Ninalala na kupata usingizi kwa amani; wewe peke yako, ee Yawe, unaniweka salama. Kwa mukubwa wa waimbaji. Kwa filimbi. Zaburi ya Daudi. Ee Yawe, usikilize maneno yangu, usikie malalamiko yangu. Usikilize kilio changu, Mufalme wangu na Mungu wangu, maana wewe ndiwe ninayekuomba. Ee Yawe, kwa mapambazuko unasikia sauti yangu, asubui ninakutolea sadaka yangu, kisha ninangojea unijibu. Wewe si Mungu anayependa ubaya; mwovu hawezi kupokelewa kwako. Wewe haupendi kuwaona wenye majivuno; wewe unawachukia wote wanaotenda maovu. Unawaangamiza wote wanaosema uongo; unawachukia wauaji na wadanganyifu. Lakini, kwa wingi wa wema wako, mimi nitaingia ndani ya nyumba yako; nitainama kwa heshima kuelekea hekalu lako takatifu. Ee Yawe, katika haki yako, uisawanishe njia yako mbele yangu. Uniongoze kwa sababu ya waadui zangu. Ndani ya vinywa vyao hamuna ukweli wowote; mioyo yao imejaa maangamizi, koo zao ni kama kaburi wazi, ndimi zao zimejaa udanganyifu. Ee Mungu, uwaazibu kwa makosa yao, waanguke katika mipango yao wenyewe; uwafukuze inje kwa sababu ya zambi zao nyingi, kwa sababu wamekuasi wewe. Lakini wanaokimbilia kwako wafurahi wote, waimbe kwa shangwe siku zote. Uwalinde wanaolipenda jina lako, kusudi wapate kushangilia kwa sababu yako. Maana wewe Yawe unawabariki watu wa haki; unawakinga kwa upendo wako kama kwa ngao. Kutoka Mukubwa wa waimbaji: kwa vyombo vyenye nyuzi nane. Zaburi ya Daudi. Ee Yawe, usiniazibu kwa hasira yako, usiniadibishe kwa kasirani yako. Unihurumie, ee Yawe, nimeishiwa nguvu; uniponyeshe, ee Yawe, ninatetemeka mpaka katika mifupa. Ninahangaika sana ndani ya roho yangu. Ee Yawe, utakawia mpaka wakati gani? Unigeukie, ee Yawe, uniokoe; uniponyeshe kwa sababu ya wema wako. Huko kwa wafu hakuna anayekukumbuka; katika kuzimu ni nani anayeweza kukusifu? Ninatabanika kwa kulia kwa uchungu; usiku ninalowanisha kitanda changu kwa machozi; kwa kulia kwangu ninalowanisha matandiko yangu. Macho yangu yamechoka kwa huzuni; yamefifia kwa kutaabishwa na waadui. Muondoke karibu nami, enyi wote watenda maovu! Maana Yawe amesikia kilio changu. Yawe amesikia ombi langu; Yawe amekubali maombi yangu. Waadui zangu wote watafezeheka na kufazaika; watarudi nyuma na kufezeheka kwa rafla. Kwa mukubwa wa waimbaji. Wimbo wa malalamiko ya Daudi, aliomwimbia Yawe kwa ajili ya Kushi wa kabila la Benjamina. Ee Yawe, Mungu wangu, ninakukimbilia wewe. Uniokoe kutoka wote wanaonitesa, uniponyeshe. Kama si vile, watakuja kunirarua kama simba, kunipasua vipandevipande wala hakuna wa kuniokoa. Ee Yawe, Mungu wangu! Kama nimetenda moja ya mambo haya: kama nimechafua mikono yangu kwa ubaya, kama nimemurudishia rafiki yangu mabaya pahali pa mema, au nimemunyanganya adui yangu bila sababu, basi, adui anifuatilie na kunikamata, akomeshe maisha yangu na kuuzika uzima wangu ndani ya mavumbi. Ee Yawe, kwa hasira yako, simama sasa ukomeshe kasirani ya waadui zangu! Amuka, ee Mungu wangu, wewe umeamuru haki ifanyike. Ukusanye mataifa kandokando yako, nawe uyatawale tokea kule juu. Wewe, ee Yawe, unayehukumu mataifa, unihukumu kadiri ya haki yangu, kulingana na ukamilifu wangu. Ukomeshe uovu wa watu wabaya, uwaimarishe watu wa haki, ee Mungu unayetenda haki, unayejua siri za mioyo na mafikiri ya watu. Mungu ndiye ngao yangu; yeye anawaokoa watu wenye moyo wa usawa. Mungu ni mwamuzi wa haki; kila siku analaumu maovu. Watu wasipogeuka toka ubaya wao, Mungu atanoa upanga wake; atavuta upinde wake na kupima shabaha. Atatayarisha silaha zake za hatari, na kuitia mishale yake moto. Mutu mubaya anatunga uovu, anajaa uharibifu na kuzaa udanganyifu. Anachimba shimo, na kulirefusha, kisha anatumbukia humo yeye mwenyewe. Uharibifu wake utamurudilia yeye mwenyewe; ukali wake utamwangukia yeye mwenyewe. Nitamushukuru Yawe kwa sababu ya haki yake; nitaimba sifa za jina la Yawe, Mungu Mukubwa. Kwa mukubwa wa waimbaji. Kwa mutindo wa watu wa Gati. Zaburi ya Daudi. Ee Yawe, Bwana wetu, jina lako linatukuzwa sana katika dunia yote! Utukufu wako unaenea mpaka juu ya mbingu! Kutoka maneno ya watoto wadogo, hata wachanga, unaimarisha nguvu mbele ya waadui zako na kuwakomesha waasi na wapinzani wako. Nikiangalia mbingu uliyoumba kwa vidole vyako, mwezi na nyota ulizozisimika huko, mutu ni nini, ee Mungu, hata umufikirie? Mwanadamu ni nini hata umujali? Umemufanya kuwa karibu sawa na Mungu, umemujaza utukufu na heshima. Ulimupa utawala juu ya vyote ulivyoviumba; uliweka viumbe vyote chini ya mamlaka yake: kondoo, ngombe, na nyama wa pori, ndege, samaki, na viumbe vyote vya bahari. Ee Yawe, Bwana wetu, jina lako linatukuzwa sana katika dunia yote! Kwa mukubwa wa waimbaji. Kwa mutindo wa wimbo “Kilio cha mwana.” Nitakushukuru wewe Mungu kwa moyo wangu wote; nitayaeleza matendo yako yote ya ajabu. Nitafurahi na kushangilia kwa ajili yako; nitaliimbia sifa jina lako, ewe Mungu Mukubwa. Waadui zangu walirudi nyuma, walijikwaa na kuangamia mbele yako. Umeitetea haki yangu katika maneno yangu; umeikaa katika kiti chako cha kifalme, wewe mwamuzi wa haki. Umeyakaripia mataifa, umewaangamiza waovu; umeyafuta majina yao kwa milele. Waadui wameangamia milele; umeiongoa miji yao, ukumbusho wao umetoweka. Lakini Yawe anatawala milele; ameweka kiti chake cha kifalme, apate kuhukumu. Anauhukumu ulimwengu kwa haki; anayaamua mataifa kama vile inavyofaa. Yawe ni kikingio cha watu wanaoonewa; yeye ni kikingio katika nyakati za taabu. Wanaojua jina lako, wanakutegemea, kwa maana wewe, ee Yawe, hauwatupi wanaokutafuta. Mumwimbie sifa Yawe anayekaa Sayuni! Muyatangazie mataifa mambo aliyotenda! Mungu analipiza kisasi cha damu iliyomwangwa; wala hasahau hata kidogo kilio cha wenye kuonewa. Ee Yawe, wewe unayeniopoa kutoka nguvu za kifo, uangalie mateso wale wanaonichukia wanayoniletea na kunirehemu kusudi nitangaze sifa zako mbele ya watu wa Sayuni, nipate kushangilia kwa sababu umeniokoa. Mataifa yameanguka katika shimo walilochimba, miguu yao imenaswa kwenye wavu waliotega. Yawe amejitambulisha; anatoa hukumu. Waovu wamenaswa kwa matendo yao wenyewe. Waovu wataishia katika kuzimu; ndiyo mataifa yote yanayomusahau Mungu. Lakini wakosefu hawatasahauliwa siku zote; tumaini la wamasikini halitapotea milele. Ee Yawe, simama sasa mwanadamu asishinde! Uyakusanye sasa hivi mataifa mbele yako, uyahukumu. Uyatie hofu, ee Yawe, watu wa mataifa watambue kwamba wao ni watu tu! Ee Yawe, mbona unasimama mbali? Kwa nini unajificha wakati tuko katika taabu? Waovu wanatesa wamasikini kwa kiburi. Mitego yao iwanase wao wenyewe! Mwovu anajisifia tamaa zake mbaya, anapata faida kwa njia mbaya, anazarau na kumukataa Yawe. Katika majivuno yake anasema: “Mungu hatagundua. Hakuna Mungu.” Hayo ndiyo mawazo yake yote. Njia za mwovu zinafanikiwa siku zote; hukumu zako ziko mbali na mawazo yake, na anazarau waadui zake wote. Anawaza ndani ya moyo: “Sitakuwa na wasiwasi; sitapatwa na taabu katika maisha.” Kinywa chake kimejaa laana, udanganyifu na ukorofi; ni mwepesi kusema maneno ya kuchukiza na maovu. Anajificha karibu na vijiji akivizia, amwue kwa siri mutu asiyekuwa na kosa. Yuko macho kumuvizia muzaifu; anajificha katika maficho yake kama simba. Anavizia apate kuwakamata wamasikini; anawanasa kwa mutego wake na kuwachukua. Muzaifu anashambuliwa na kuangushwa chini; anaangushwa kwa ukali wa mutu mwovu. Mwovu anawaza ndani ya moyo wake: “Mungu amesahau; ameficha uso wake, haoni kitu!” Ee Yawe, simama sasa uwaazibu! Usiwasahau wanaoteswa. Ee Mungu, kwa nini mwovu anakuzarau, na kusema kwamba wewe haujali kitu? Lakini wewe unawaona wenye taabu na shida; nawe uko tayari kuwasaidia siku zote. Muzaifu anakutegemea wewe, ee Mungu, wewe umekuwa siku zote musaada wa yatima. Uvunje nguvu za mutu mwovu; ukomeshe uovu wake wote, usikuwe tena. Yawe ni mufalme milele na milele! Mataifa yatatoweka katika inchi yake. Ee Yawe, unapokea maombi ya muzaifu; unamutia moyo na kumutegea sikio. Utawatendea haki wayatima na wanaoteswa, mwanadamu anayekuwa mavumbi asiweze tena kuleta hofu. Kwa mukubwa wa waimbaji. Zaburi ya Daudi. Yawe ni kimbilio langu; namna gani basi munaweza kuniambia: “Ruka kama ndege, mpaka kwenye milima, maana waovu wanavuta pinde; wameweka mishale tayari juu ya kamba, kusudi wawapige mishale watu wenye moyo wa usawa katika giza! Kama misingi ikiharibiwa, mutu wa haki atafanya nini?” Yawe yuko katika hekalu lake takatifu; kiti cha kifalme cha Yawe kiko mbinguni. Kwa macho yake anawachungulia wanadamu, na kujua kila kitu wanachofanya. Yawe anawapima watu wa haki na waovu; anawachukia wanaopenda kutesa kwa ukali. Atawanyeshea waovu makaa ya moto na kiberiti; upepo mukali utakuwa ndio azabu yao. Yawe ni wa haki na anapenda watu watende kwa haki. Watu wa usawa wataona uso wake. Kwa mukubwa wa waimbaji. Kwa vyombo vyenye nyuzi nane. Zaburi ya Daudi. Unisaidie, ee Yawe! Watu wema wamekwisha; waaminifu wametoweka kati ya watu. Kila mumoja anamudanganya mwenzake; anabembeleza lakini ni kwa moyo wa unafiki. Ee Yawe, ukomeshe midomo hiyo ya kudanganya, na ndimi hizo zinazojigamba. Wao wanasema: “Kwa ndimi zetu tutashinda; tuko na midomo, nani anayeweza kututawala?” Lakini Yawe anasema: “Kwa sababu wamasikini wanaugua, na wakosefu wanalia, sasa ninasimama, nami nitawapa usalama wanaoutazamia.” Ahadi za Yawe ni safi, safi kama feza iliyosafishwa katika chungu, kama feza iliyosafishwa mara saba. Utulinde, ee Yawe, utukinge siku zote na kizazi hiki kiovu. Waovu wanazunguka popote; upotovu unatukuzwa kati ya watu. Kwa mukubwa wa waimbaji. Zaburi ya Daudi. Mpaka wakati gani, ee Yawe, utaendelea kunisahau? Mpaka wakati gani utanificha uso wako? Mpaka wakati gani nitakuwa na wasiwasi katika roho na sikitiko katika moyo siku hata siku? Mpaka wakati gani waadui zangu watanishinda? Uniangalie na kunijibu, ee Yawe, Mungu wangu. Uyaangazie macho yangu, nisipatwe na usingizi wa kifo. Usiwaache waadui zangu waseme: “Tumemushinda huyu!” Watesaji wangu wasifurahie kuanguka kwangu. Lakini mimi ninatumainia wema wako, moyo wangu ufurahie wokovu wako. Nitakuimbia wewe, ee Yawe, kwa vyote ulivyonitendea! Kwa mukubwa wa waimbaji. Zaburi ya Daudi. Mupumbafu anajisemesha hivi katika moyo: “Hakuna Mungu.” Wote wamepotoka kabisa, matendo yao ni ya kuchukiza; hakuna hata mumoja anayetenda mazuri! Yawe anawaangalia wanadamu kutoka mbinguni aone kama kuna yeyote mwenye akili, kama kuna yeyote anayemutafuta Mungu. Lakini wote wamekosa, wote wamepotoka pamoja; hakuna anayetenda mazuri, hakuna hata mumoja. Hao wanaotenda maovu hawajui kitu? Wanatafuna watu wangu kama mikate, wala hawajali Yawe. Hapo watashikwa na hofu, maana Mungu ni pamoja na watu wa haki. Unaweza kuvuruga mipango ya masikini, lakini Yawe ndiye kimbilio lake. Heri ukombozi wa Israeli ungefika kutoka Sayuni! Yawe atakapotengeneza hali ya watu wake, wazao wa Yakobo watashangilia; watu wa Israeli watafurahi. Zaburi ya Daudi. Ee Yawe, nani atakayekaa katika hema yako? Nani atakayeishi juu ya mulima wako mutakatifu? Mashairi ya Daudi. Unilinde, ee Mungu, maana ninakimbilia kwako. Ninamwambia Mungu: “Wewe ni Bwana wangu; sina uheri wowote isipokuwa wewe.” Na juu ya waaminifu katika inchi, ninaheshimu nguvu zao. Lakini wanaoabudu miungu mingine, watapata mateso mengi. Sitaitolea sadaka za damu hata kidogo, na majina ya miungu hiyo sitayataja. Wewe, ee Yawe, ndiwe riziki yangu kubwa, majaliwa yangu yako katika mikono yako. Umenipimia sehemu nzuri sana; urizi wangu ni wa kupendeza. Ninamusifu Yawe anayeniongoza. Usiku zamiri yangu inanifundisha. Siku zote Yawe ni mbele yangu; yeye yuko pamoja nami, wala sitatikisika. Kwa hiyo nitafurahi kwa moyo wote na kushangilia, nami nitakaa salama kabisa. Kweli wewe unanikinga na nguvu za kuzimu, haumwachi mutakatifu wako aone kaburi. Unanionyesha njia ya kufikia uzima. Kuwa mbele yako ni kujazwa furaha, kuwa kwa kuume kwako kunapendeza milele. Maombi ya Daudi. Ee Yawe, usikie ombi langu la haki, usikilize kilio changu, uyategee sikio maombi yangu yasiyokuwa ya udanganyifu. Haki yangu ikuje kutoka kwako, maana wewe unajua jambo la haki. Wewe unajua kabisa moyo wangu; umenifikia usiku kunichunguza, umenitia katika majaribu; haukuona uovu ndani yangu, sikusema kitu kisichofaa. Juu ya matendo watu wanayotenda, mimi nimetii amri yako, sikushika njia za watesaji wakali. Nimefuata siku zote njia yako; wala sijatereza hata kidogo. Ee Mungu, ninakuita, maana wewe unanijibu; unitegee sikio, uyasikie maneno yangu. Onyesha wema wako wa ajabu; uwaokoe kutoka waadui zao wale wanaokimbilia kwako. Unilinde kama mboni ya jicho lako; unifiche chini ya kivuli cha mabawa yako, mbali na mashambulio ya waovu, mbali na waadui zangu wa hatari wanaonizunguka. Hao hawana huruma yoyote ndani ya moyo; wamejaa maneno ya kujivuna. Wananifuatilia na kunizunguka; wananivizia waniangushe chini. Wako tayari kunirarua kama simba, kama simba mukali anavyovizia nyama. Ee Yawe, simama sasa uwapiganishe na kuwaporomosha! Kwa upanga wako uokoe nafsi yangu kutoka waovu. Ee Yawe, mukono wako uwafukuze kati ya watu, tukio lao likuwe kutengana na wanaokuwa wazima. Uwashibishe kwa akiba uliyowawekea, watoto wao nao washibe na kuacha sehemu, wawaachie hata na wajukuu wao. Lakini mimi nitauona uso wako, maana mimi ni mutu wa haki; nitakapoamuka nitajaa furaha kwa sababu unanitokea. Kwa mukubwa wa waimbaji. Zaburi ya Daudi, mutumishi wa Mungu, aliyomwimbia wakati alipomwokoa katika mikono ya Saulo na waadui wengine. Ninakupenda, ee Yawe, nguvu yangu! Yawe ni kikingio changu, kimbilio langu, mukombozi wangu, Mungu wangu, yule ambaye ninamukimbilia, ngao yangu, nguvu ya wokovu wangu, munara wangu. Ninamwita Yawe anayestahili sifa anisaidie, nami ninaokolewa kutoka waadui zangu. Kamba za kifo zilinizunguka, mafuriko ya maangamizi yalinishambulia; kamba za kuzimu zilinizunguka, mitego ya kifo ilikuwa mbele yangu. Katika taabu yangu, nilimwita Yawe; nilimulilia Mungu wangu anisaidie. Toka katika hekalu lake, alisikia sauti yangu; kilio changu kilimufikia katika masikio yake. Halafu dunia ikatetemeka na kutikisika, misingi ya milima ikayumbayumba na kutetemeka, kwa maana Mungu alikuwa amekasirika. Moshi ulifuka kutoka katika pua lake, moto wenye kuteketeza ukatoka katika kinywa chake, makaa ya moto yakatokea. Aliinamisha anga, akashuka chini, na wingu jeusi lilikuwa chini ya miguu yake. Alipanda juu ya kerubi na kuruka, akaruka juu ya mabawa ya upepo. Alijifunika giza pande zote, alijizungushia mawingu mazito ya mvua. Umeme ulimetameta mbele yake; na katika mawingu kukatokea mvua ya mawe na makaa ya moto. Yawe alinguruma kutoka mbingu; Mungu Mukubwa akatoa sauti yake. Aliwapiga waadui mishale yake, akawatawanya; alirusha umeme mukali, akawakimbiza. Ee Yawe, ulipovikaripia, pumzi ya pua yako ilifunua vilindi vya bahari na misingi ya dunia ikaonekana. Mungu alinyoosha mukono wake kutoka juu, akanitwaa, alininyanyua kutoka ndani ya maji mengi. Aliniokoa kutoka adui yangu mwenye nguvu, kutoka hao walionichukia na kuwa na nguvu kunishinda. Walinishambulia nilipokuwa katika taabu, lakini Yawe alinikinga. Alinileta, akaniweka kwenye nafasi ya usalama; aliniponyesha kwa sababu alipendezwa nami. Yawe alinitendea kwa kadiri ya haki yangu; alinilipa kwa vile mikono yangu haina kosa. Maana nimefuata njia za Yawe, wala sikujitenga na Mungu wangu kwa ajili ya uovu. Nimeshika maagizo yake yote, sikuacha kufuata masharti yake. Mbele yake nilikuwa mukamilifu; nimejikinga nisikuwe na kosa. Yawe amenilipa kwa kadiri ya haki yangu; kwa kadiri ya usafi wa mikono yangu mbele yake. Wewe ni mwema kwa wema, mukamilifu kwa wakamilifu, bila kosa kwa wale ambao hawafanyi makosa, lakini mukali kwa waovu. Wewe unawaokoa wanyenyekevu, lakini unawashusha wenye macho ya kujivuna. Wewe, ee Yawe, unawakisha taa yangu. Mungu wangu anafanya giza langu likuwe mwangaza. Kwa musaada wako, ninashinda kundi la waaskari; kwa musaada wa Mungu wangu, ninaruka kuta. Njia ya Mungu ni kamilifu. Ahadi ya Yawe ni ya kuaminika. Yeye ni ngao kwa wote wanaomukimbilia. Nani anayekuwa Mungu isipokuwa Yawe? Nani anayekuwa kikingio isipokuwa Mungu wetu? Ni Mungu ambaye ananipatia nguvu, na kuifanya salama njia yangu. Ameiimarisha miguu yangu kama ya swala, na kunilinda salama juu ya milima. Ananifundisha kupigana vita, mikono yangu iweze kuvuta upinde wa chuma. Umenipa ngao yako ya wokovu na kuniimarisha kwa mukono wako wa kuume. Nimefanikiwa kwa sababu ulikubali kunisaidia. Umepanua njia yangu wala miguu yangu haikuteleza. Niliwafuata waadui zangu na kuwakamata; sikurudi nyuma mpaka wamemalizika. Niliwaangamiza, wasiweze kuinuka tena; walianguka chini ya miguu yangu. Wewe ulinijalia nguvu ya kupigana vita; uliwaporomosha waadui chini yangu. Uliwakimbiza waadui zangu, na wale walionichukia niliwaangamiza. Walitafuta musaada, lakini hakukukuwa wa kuwasaidia; walimulilia Yawe, lakini hakuwajibu. Niliwatwanga, wakakuwa kama vumbi inayopeperushwa na upepo; niliwakanyaga kama matope katika barabara. Wewe uliniokoa kutoka mashambulizi ya watu, ukanifanya kuwa mutawala wa mataifa. Watu nisiowajua walinitumikia. Waliposikia tu habari zangu, walinitii; wageni walinijia wakinyenyekea. Wageni walivunjika moyo; wakakuja kutoka makimbilio yao wakitetemeka. Yawe anaishi! Yeye ni kikingio changu – asifiwe! Mungu ni mwokozi wangu – atukuzwe! Yeye ameniwezesha kulipiza kisasi; na kuwaweka mataifa chini ya mamlaka yangu. Ameniokoa kutoka waadui zangu, Ee Yawe, ulinitukuza juu ya wapinzani wangu na kuniponyesha kutoka watesaji wakali. Kwa hiyo, nitakutukuza kati ya mataifa, nitaliimbia sifa jina lako. Mungu anamujalia mufalme wake ushindi mukubwa; anamutendea mema muchaguliwa wake, ndiye Daudi na wazao wake milele. Kwa mukubwa wa waimbaji. Zaburi ya Daudi. Mbingu zinatangaza utukufu wa Mungu; anga linaeleza kazi ya mikono yake. Muchana unaupasha habari muchana unaofuata, usiku unaufahamisha usiku unaofuata. Si kwa musemo au kwa maneno; wala hakuna sauti inayosikilika; hata hivyo, ujumbe wao unaenea katika dunia yote, na habari zao zinafika miisho ya ulimwengu. Mungu amewekea jua makao yake katika anga; nalo linatoka kama vile bwana-arusi kutoka chumba chake, linakimbia kwa furaha katika njia yake kama shujaa. Linatokea kwa upande mumoja, na kuzunguka mpaka upande mwingine; hakuna kinachoweza kuepuka joto lake. Sheria ya Yawe ni kamilifu; inamupa mutu uzima mupya. Maagizo ya Yawe ni ya kuaminiwa; yanawapa wajinga hekima. Kanuni za Yawe ni sawa; zinafurahisha moyo. Amri za Yawe ni safi; zinamufungua mutu macho. Kumutii Yawe ni jambo jema; kunadumu milele. Maagizo ya Yawe ni sawa, yote ni ya haki kabisa. Yanatamanika kuliko zahabu, kuliko zahabu safi kabisa. Ni matamu kuliko asali, kuliko asali safi kabisa. Yananifundisha mimi mutumishi wako; kuyafuata kunaniletea zawadi kubwa. Lakini nani anayeona makosa yake mwenyewe? Ee Mungu, unisamehe makosa nisiyoyajua. Unikinge mimi mutumishi wako na makosa ya makusudi, usikubali hayo yanitawale. Hapo nitakuwa mukamilifu, wala sitakuwa na kosa kubwa. Maneno ya kinywa changu, na mawazo ya moyo wangu, yakubalike mbele yako, ee Yawe, kikingio changu na mwokozi wangu! Kwa mukubwa wa waimbaji. Zaburi ya Daudi. Yawe akujibu unapokuwa katika taabu; jina la Mungu wa Yakobo likulinde. Akupelekee musaada kutoka katika hekalu lake; akukinge tokea kwenye mulima Sayuni. Akumbuke sadaka zako zote; akubali sadaka zako za kuteketezwa. Akujalie unayotamani ndani ya moyo wako, afanikishe mipango yako yote. Tutashangilia kwa ajili ya ushindi wako; tutainua bendera kwa kutukuza jina la Mungu wetu. Yawe akutimizie mapenzi yako yote! Ninajua Yawe atamusaidia mufalme aliyemuchagua, atamujibu tokea pahali pake patakatifu mbinguni; kwa mukono wake wenye nguvu atamujalia ushindi mukubwa. Wamoja wanajivunia magari ya vita, wengine farasi wao. Lakini sisi tunajivunia Yawe, Mungu wetu. Hao wanajikwaa na kuanguka; lakini sisi tunasimama na kuimarika. Ee Yawe, umujalie mufalme ushindi, utujibu wakati tunapokuomba. Kwa mukubwa wa waimbaji. Zaburi ya Daudi. Ee Yawe, mufalme anashangilia kwa nguvu yako, anafurahi sana kwa musaada uliomupa. Umemutimizia mapenzi ya moyo wake; wala haukumukatalia ombi lake. Umemufikia, ukamupatia baraka nzurinzuri; umemuvalisha taji ya zahabu safi juu ya kichwa chake. Alikuomba maisha, nawe ukamupatia; ulimupatia siku nyingi milele na milele. Kwa musaada wako, amepata utukufu sana; wewe umemujalia sifa na heshima. Unamujalia baraka zako siku zote; unamufurahisha kwa sababu uko pamoja naye. Mufalme anamutumainia Yawe; kwa wema wa Mungu Mukubwa atakuwa salama. Mukono wako, ewe mufalme, utawakamata waadui zako wote; mukono wako wa nguvu utawakamata wanaokuchukia. Utakapotokea utawaangamiza kama kwa moto wa furu. Yawe atawamaliza kwa hasira yake, moto utawateketeza kabisa. Utawaangamiza wazao wao watoweke katika dunia; watoto wao hawatabaki kati ya wanadamu. Hata kama wakifanya shauri baya juu yako, kama wakikamata mipango ya udanganyifu, hawataweza kitu hata kidogo. Kwa maana wewe utapiga mishale mbele yao, utawakimbiza mbio. Utukuzwe, ee Yawe, kwa sababu ya nguvu yako! Tutaimba na kusifu kwa ajili ya uwezo wako. Kwa mukubwa wa waimbaji. Mutindo wa wimbo “Swala wa mapambazuko”. Mungu wangu, Mungu wangu, mbona umeniacha? Mbona uko mbali sana kwa kunisaidia, mbali na maneno ya kilio changu? Ee Mungu wangu, ninakulilia muchana lakini haujibu; ninakulalamikia usiku, lakini sipumziki. Hata hivyo, wewe ni mutakatifu; wewe unatawala na kusifiwa na Waisraeli. Babu zetu walikutegemea; walikutegemea, nawe ukawaokoa. Walikulilia wewe, wakaokolewa; walikutegemea, nao hawakufezeheka. Lakini mimi ni mududu tu, wala si mutu; nimetukaniwa na kuzarauliwa na watu. Wote wanaoniona wananichekelea; wananizomea na kutikisa vichwa vyao. Wanasema: “Alimutegemea Yawe, basi, Mungu amuponyeshe! Kama Mungu anapendezwa naye, basi, amwokoe!” Lakini wewe ndiwe uliyenitoa katika tumbo la mama yangu, uliniweka salama kwa kifua cha mama yangu. Nimekutegemea tangu kuzaliwa kwangu. Tangu nilipozaliwa, wewe umekuwa Mungu wangu. Usikae mbali nami, kwa maana taabu imekaribia; wala hakuna wa kunisaidia. Waadui wengi wananizunguka kama ngombe dume; wamenisonga kama ngombe dume wanono wa Basani! Wanafungua vinywa vyao kama simba, tayari kushambulia na kurarua. Nimekwisha kama maji yaliyomwangika; mifupa yangu yote imeteguka; moyo wangu ni kama inta, unayeyuka ndani yangu. Koo langu limekauka kama kigae; ulimi wangu unanata ndani ya kinywa changu. Wewe umenilaza pembeni ya kaburi. Kundi la waovu limenizunguka; wananizunguka kama kundi la imbwa; wamenitoboa mikono na miguu. Nimebaki mifupa mitupu; waadui zangu wananiangalia na kunisimanga. Wanagawanya nguo zangu, na kuipigia kanzu yangu kura. Lakini wewe, ee Yawe, usikae mbali nami. Ukuwe musaada wangu, ukuje haraka kunisaidia. Uokoe nafsi yangu toka upanga, uokoe maisha yangu toka mikono ya imbwa hao! Uniokoe toka kinywa cha simba; uokoe nafsi yangu zaifu toka pembe za mbogo hao. Nitawaelezea wandugu zangu matendo yako; nitakusifu kati ya kusanyiko lao, nikisema: “Enyi munaomwabudu Yawe, mumusifu! Mumutukuze, enyi wazao wote wa Yakobo! Mumwogope Mungu, enyi wazao wote wa Israeli! Maana yeye hatupilii au kuzarau taabu ya muzaifu; wala hajifichi mbali naye, lakini anamusikiliza anapomwomba musaada.” Kwa sababu yako ninakusifu katika kusanyiko kubwa la watu; nitatimiza ahadi zangu mbele ya wanaomwabudu. Wamasikini watakula na kushiba; wanaomutafuta Yawe watamusifu. Mungu awajalie waishi milele! Ulimwengu wote utakumbuka na kumurudilia Yawe; jamaa zote za mataifa zitamwabudu. Maana Yawe ni mufalme; yeye anatawala mataifa. Wenye kiburi wote katika dunia watamwabudu; wote ambao ni wa kufa watainama mbele yake, wote ambao hawawezi kudumisha uzima wao. Vizazi vyao vitamutumikia; watu wataelezea kizazi kinachokuja habari za Yawe, watatangazia wale watakaozaliwa matendo yake ya wokovu. Watu wasiozaliwa bado wataambiwa: “Yawe ndiye aliyefanya hayo!” Zaburi ya Daudi. Yawe ni muchungaji wangu; sitapungukiwa na kitu. Ananipumzisha kwenye majani mabichi; ananiongoza kando ya maji matulivu, na kuirudishia nafsi yangu nguvu mupya. Ananiongoza katika njia sawa kwa utukufu wa jina lake. Hata nikipita katika bonde la giza kubwa, sitaogopa hatari yoyote, maana wewe, ee Yawe, ni pamoja nami; gongo lako na fimbo yako vinanipa moyo. Umenitayarishia karamu mbele ya waadui zangu. Umekipakaa kichwa changu mafuta. Kikombe changu umekijaza tele. Kweli, uzuri na wema wako vitakuwa pamoja nami siku zote za maisha yangu; nami nitakaa katika nyumba ya Yawe milele. Zaburi ya Daudi. Dunia na vyote vinavyokuwa ndani yake ni vya Yawe; ulimwengu na wote wanaoishi ndani yake ni mali yake. Maana yeye aliweka misingi ya dunia juu ya bahari; aliisimika imara juu ya maji mengi. Nani atakayepanda kwa mulima wa Yawe? Nani atakayekaa katika hekalu lake takatifu? Ni mutu wa matendo mema na moyo safi, asiyefuata mambo ya ovyo, wala kuapa kwa uongo. Mutu huyo atapokea baraka kwa Yawe, na haki yake kwa Mungu mwokozi wake. Ndiyo hali ya kizazi cha watu wanaomutafuta yeye, watu wanaomutafuta Mungu wa Yakobo. Mufunguke, enyi milango; mufunguke, enyi milango ya tangia zamani, kusudi Mufalme mwenye utukufu aingie. Ni nani huyo Mufalme mwenye utukufu? Ni Yawe, mwenye nguvu na uwezo; Yawe, mwenye uwezo katika vita. Mufunguke, enyi milango, mufunguke, enyi milango ya tangia zamani, kusudi Mufalme mwenye utukufu aingie. Ni nani huyo Mufalme mwenye utukufu? Ni Yawe, wa majeshi, yeye ndiye Mufalme mwenye utukufu. Zaburi ya Daudi. Ee Yawe, ninakutolea moyo wangu. Ninakutumainia wewe, ee Mungu wangu, usiniache nifezeheke; waadui zangu wasifurahie kushindwa kwangu. Usimwache anayekutumainia kupata haya; lakini wafezeheke wote wanaokuasi kwa makusudi. Unijulishe njia zako, ee Yawe; unifundishe nifuate unayotaka. Uniongoze katika ukweli wako na kunifundisha, kwa maana wewe ni Mungu, mwokozi wangu; ninakutegemea wewe kila siku. Ee Yawe, ukumbuke rehema yako na wema wako ambazo ni za milele. Usikumbuke zambi na makosa ya ujana wangu; unikumbuke kwa kadiri ya wema wako, kwa ajili ya uzuri wako, ee Yawe. Yawe ni muzuri na wa usawa, kwa hiyo anawafundisha wakosaji njia. Anawaongoza wanyenyekevu katika haki; anawafundisha njia yake. Njia zote za Yawe ni njema na za uaminifu kwa wale wanaoshika agano lake na maagizo yake. Kwa ajili ya jina lako, ee Yawe, unisamehe kosa langu, kwa maana ni kubwa. Kila mutu anayemwabudu Yawe, Yawe atamufundisha njia ya kufuata. Mutu wa namna hiyo atafanikiwa siku zote, na wazao wake watarizi inchi. Yawe ni rafiki ya wale wanaomwabudu; yeye anawajulisha agano lake. Ninainua macho kwa Yawe siku zote; yeye ataopoa miguu yangu kutoka mutego. Unielekee, ee Mungu, unionee huruma, maana mimi ni pekee na zaifu. Uniondolee mahangaiko ya moyo wangu; uniondoe katika mashaka yangu. Uangalie mateso yangu na taabu yangu; unisamehe zambi zangu zote. Angalia jinsi waadui zangu wanavyokuwa wengi; ona jinsi wanavyonichukia vikali. Uyalinde maisha yangu, uniokoe; ninakukimbilia wewe, usikubali nifezeheke. Ukamilifu na usawa vinanikinga, maana ninakutumainia wewe. Ee Mungu, uwaokoe watu wako, Israeli; uwaokoe kutoka taabu zao zote. Zaburi ya Daudi. Ee Yawe, unitetee, maana nimeishi katika ukamilifu, nimekutumainia wewe bila kusita. Unijaribu, ee Yawe, na kunipima; uchunguze moyo wangu na akili yangu. Wema wako uko mbele ya macho yangu, ninaishi kutokana na uaminifu wako. Sikusanyiki na watu wapotovu; sishirikiani na watu wanafiki. Ninachukia mikutano ya wabaya; wala sitakusanyika na waovu. Ninanawa mikono yangu kuonyesha kama sina kosa, na kuizunguka mazabahu yako, ee Yawe, nikiimba wimbo wa shukrani, na kueleza matendo yako ya ajabu. Ee Yawe, ninapenda makao yako, pahali utukufu wako unapokaa. Usiniangamize pamoja na wenye zambi, wala usinitupe pamoja na wauaji, watu ambao matendo yao ni maovu kila wakati, watu ambao wanapokea kituliro kila wakati. Lakini mimi ninaishi katika ukamilifu; unihurumie na kunikomboa. Mimi nimesimama pahali penye kuwa imara; nitamusifu Yawe katika kusanyiko kubwa. Zaburi ya Daudi. Yawe ni mwangaza wangu na wokovu wangu, ni nani nitakayemwogopa? Yawe ni mulinzi wa maisha yangu, sitamwogopa mutu yeyote. Waovu wakinishambulia, na kutaka kuniangamiza, hao wapinzani wangu watajikwaa na kuanguka. Hata jeshi likinizunguka, moyo wangu hautaogopa kitu; hata nikishambuliwa kwa vita, sitakata tumaini. Jambo moja nimemwomba Yawe, ninatafuta hili tu: nikae ndani ya nyumba ya Yawe siku zote za maisha yangu, niuone uzuri wa Yawe, na kutafuta maongozi yake ndani ya hekalu lake. Siku ya taabu atanificha ndani ya nyumba yake; atanificha katika hema lake, atanilinda salama juu ya mulima. Nami nitawaangalia kwa majivuno waadui zangu wanaonizunguka. Nitamutolea Yawe sadaka kwa shangwe, ndani ya hekalu lake, nitaimba na kumushangilia. Usikie, ee Yawe, ninapokulilia, unionee huruma na kunijibu. Moyo wangu unaniambia: “Kuja umutafute Mungu!” Basi, ninakutafuta, ee Yawe. Usinigeuzie mugongo, usinikatae kwa hasira mimi mutumishi wako. Wewe umekuwa siku zote musaada wangu. Usinitupe wala usiniachilie, ee Mungu Mwokozi wangu. Hata kama wazazi wangu wakinitupa, Yawe atanipokea kwake. Unifundishe njia yako, ee Yawe. Uniongoze katika njia inayokuwa sawa kwa sababu ya waadui zangu. Usiniache waadui wanitendee wanavyopenda; maana washuhuda wa uongo wananiinukia, nao wanatoa vitisho vyao vikali. Ninaamini kwamba nitauona uzuri wa Yawe katika makao ya wazima. Umutegemee Yawe! Ujitie moyo, ukuwe hodari! Umutegemee Yawe! Zaburi ya Daudi. Ninakulilia, ee Yawe! Ewe kikingio changu, usikuwe kama kiziwi kwangu. Usikuwe kama haunisikilizi, nisikuwe kama wale wanaoshuka katika shimo la wafu. Sikiliza sauti ya ombi langu, ninapokulilia unisaidie, ninapoinua mikono yangu kuelekea hekalu lako takatifu. Usiniazibu pamoja na watu wabaya, wale watenda maovu wanaosema vizuri na wenzao, kumbe wanajaa ubaya ndani ya moyo. Uwalipe kwa kadiri ya matendo yao, kufuatana na maovu waliyotenda. Uwalipe kwa kadiri ya matendo yao wenyewe; uwatendee yale wanayostahili. Hawashuguliki na matendo ya Yawe; hawatambui mambo aliyofanya. Kwa sababu hiyo atawabomoa, wala hatawajenga tena upya. Atukuzwe Yawe, maana amesikiliza ombi langu. Yawe ndiye nguvu na ngao yangu; tegemeo la moyo wangu ni kwake. Amenisaidia, nami nikashangilia kwa moyo wote; kwa wimbo wangu ninamushukuru. Yawe ni nguvu ya watu wake; yeye ni kimbilio la mufalme aliyemuchagua. Ee Mungu, uwaokoe watu wako; uwabariki watu hao wanaokuwa mali yako. Ukuwe muchungaji wao na kuwalinda milele. Zaburi ya Daudi. Mumupe Yawe heshima, enyi viumbe vya mbingu, museme kwamba Yawe ni mutukufu na mwenye nguvu. Museme kwamba jina la Yawe ni tukufu. Mumwabudu katika pahali pake patakatifu. Sauti ya Yawe inasikilika juu ya maji; Mungu mutukufu anapiga radi, sauti ya Yawe inasikilika juu ya bahari! Sauti ya Yawe ni yenye nguvu, sauti ya Yawe ni yenye mamlaka. Sauti ya Yawe inavunja miti mikubwa ya mierezi; Yawe anavunja mierezi ya Lebanoni. Anarusha milima ya Lebanoni kama mwana-ngombe, milima ya Hermoni kama mwana-mbogo. Sauti ya Yawe inatokeza ndimi za moto. Sauti ya Yawe inatetemesha jangwa, Yawe anatetemesha jangwa la Kadesi. Sauti ya Yawe inatikisa mivule, inaongoa majani ya miti ya pori, na wote wanaokuwa katika hekalu lake wanasema: “Utukufu kwa Mungu!” Yawe ameikaa juu ya mafuriko ya maji; Yawe ni mufalme anayetawala milele. Yawe awape watu wake nguvu! Yawe awabariki watu wake kwa amani! Mashairi yanayoelekea muzinduo wa hekalu. Zaburi ya Daudi. Ninakutukuza, ee Yawe, maana umeniokoa, wala haukuwaacha waadui zangu wanisimange. Ee Yawe, Mungu wangu, nilikulilia, nawe ukaniponyesha. Ee Yawe, umeniokoa kutoka kuzimu; umenipa tena uzima, umenitoa kutoka kati ya wafu. Mumwimbie Yawe sifa, enyi waaminifu wake; mukumbuke utakatifu wake na kumushukuru. Hasira yake inadumu muda kidogo tu, upendo wake unadumu milele. Kilio kinaweza kuwa usiku, lakini muchana kunatokea furaha. Mimi nilipofanikiwa, nilisema: “Sitashindwa hata kidogo! Kwa upendo wako, ee Yawe, umeniimarisha kama mulima mukubwa.” Lakini ukajificha mbali nami, nami nikafazaika. Nilikulilia wewe, ee Yawe; nilikusihi, ee Yawe: “Utapata faida gani nikikufa na kushuka mpaka katika shimo la wafu? Mavumbi ya wafu yanaweza kukusifu? Yanaweza kusimulia uaminifu wako? Usikie, ee Yawe, unihurumie; ee Yawe, unisaidie!” Wewe umegeuza malalamiko yangu kuwa ngoma ya furaha; umeniondolea huzuni yangu, ukanijaza furaha. Mimi nitakusifu wala sitakaa kimya. Ee Yawe, Mungu wangu, nitakushukuru milele. Kwa mukubwa wa waimbaji. Zaburi ya Daudi. Kwako, ee Yawe, ninakimbilia. Usiniache nifezeheke hata kidogo; kwa haki yako, uniokoe. Unitegee sikio, uniokoe haraka! Ukuwe kwangu kikingio na kimbilio, kusudi nipate kuokoka. Wewe ni kikingio na upango wangu; kwa heshima ya jina lako, uniongoze na kunionyesha njia. Uniopoe katika mutego walionitegea; maana wewe ni mulinzi wangu. Ninaweka roho yangu katika mikono yako; umenikomboa, ee Yawe, Mungu mwaminifu. Ninawachukia wanaoabudu vitu vya bure. Mimi, ninakutumainia wewe, ee Yawe. Nitashangilia na kufurahia wema wako, maana wewe unaona taabu yangu, unajua huzuni yangu. Wewe haukunitoa katika mikono ya waadui zangu; lakini umenisimamisha kwenye pahali pa usalama. Unionee huruma, ee Yawe, niko katika taabu; macho yangu yamechoka kwa ajili ya huzuni, nimeishiwa nguvu katika mwili na roho. Maisha yangu yamekwisha kwa ajili ya kuugua; nayo miaka yangu kwa ajili ya kusikitika. Nguvu zangu zimeniishia kwa kutaabika; hata mifupa yangu imekauka. Waadui zangu wote wananizarau, na hasa zaidi wenzangu. Warafiki zangu wameniona kuwa kitisho; wanaponiona katika njia wananikimbia. Nimesahaulika kama mutu aliyekufa; nimekuwa kama chungu kilichovunjikavunjika. Ninasikia watu wakinongonezana; kuna vitisho kila upande. Wanafanya shauri baya juu yangu, wanafanya mipango ya kuniua. Lakini mimi ninakutumainia wewe, ee Yawe. Ninasema: “Wewe ni Mungu wangu!” Maisha yangu ni katika mikono yako. Uniokoe kutoka waadui zangu, uniokoe kutoka hao wanaonitesa. Uniangalie mimi mutumishi wako; uniokoe kwa wema wako. Usiniache nifezeheke, ee Yawe, maana mimi ninakulilia; lakini uwaache waovu wafezeheke, uwaache wapotelee huko kuzimu. Funga midomo ya hao watu waongo, watu wenye kiburi na majivuno, ambao wanazarau watu wa haki. Kweli, mazuri yako ni mengi sana, unayowawekea wale wanaokuabudu! Unawatendea mazuri mbele ya watu wote wale wanaokukimbilia. Unawaficha kwenye usalama pahali unapokuwa, mbali na mipango mibaya ya watu; unawalinda salama, mbali na ubishi wa waadui zao. Yawe asifiwe, maana amenionyesha wema wake wa ajabu, nilipozungukwa katika muji unaoshambuliwa. Nami niliogopa na kuzani kwamba ulikuwa umenitupa; kumbe, ulisikia kilio changu nilipokuita unisaidie. Mumupende Yawe, enyi watakatifu wake wote. Yawe anawalinda watu waaminifu; lakini anawaazibu kabisa wenye kiburi jinsi wanavyostahili. Mujitie moyo, mukuwe hodari, enyi wote munaomutumainia Yawe. Zaburi ya Daudi: Mashairi. Heri mutu aliyesamehewa kosa lake, mutu ambaye zambi yake imeondolewa kabisa. Heri mutu ambaye Yawe hamuhesabii kosa, mutu ambaye hana udanganyifu ndani ya moyo wake. Nilipokuwa sijaitikia zambi yangu, nilikuwa muzaifu sana kwa kulia muchana kutwa. Muchana na usiku mukono wako ulinilemea; nguvu zangu zikakwisha, kama maji yanavyokauka wakati wa kipwa. Kisha niliitikia makosa yangu mbele yako, wala sikuficha uovu wangu. Nilisema kwamba nitaungama makosa yangu mbele ya Yawe. Nawe ukanisamehe zambi yangu. Kwa hiyo, kila mwaminifu akutolee maombi wakati wa taabu. Mafuriko ya maji hayatamufikia. Wewe unanificha kwa kunilinda wakati wa taabu. Ninazungukwa na ukombozi wako. Mungu anasema: “Nitakufundisha na kukuonyesha njia utakayofuata. Nitakushauria kwa uangalifu mukubwa. Usikuwe mupumbafu kama farasi au nyumbu, ambao lazima wafungwe kamba ndani ya kinywa, kama sivyo hawatakukaribia.” Watu waovu watapata mateso mengi, lakini wanaomutumainia Yawe wanazungukwa na wema wake. Mufurahi na kushangilia kwa sababu ya Yawe, enyi watu wa haki; mupige vigelegele vya shangwe, enyi wenye moyo wa usawa. Mushangilie kwa sababu ya Yawe, enyi watu wa haki! Watu wa usawa ndio wanaostahili kumusifu Mungu. Mumusifu Yawe kwa zeze; mumwimbie kwa kinubi cha nyuzi kumi. Mumwimbie wimbo mupya; mupige kinubi vizuri na kushangilia. Neno la Yawe ni la usawa; na matendo yake yote ni ya kuaminika. Yawe anapenda haki na sheria. Dunia imejaa wema wake. Mbingu ziliumbwa kwa neno la Yawe, na vyote vinavyokuwa ndani yake kwa pumzi ya kinywa chake. Alikusanya maji ya bahari kama katika chupa, akavifunga vilindi vya bahari ndani ya gala. Dunia yote imwogope Yawe! Wakaaji wote wa dunia wamwabudu! Maana alisema, na ulimwengu ukakuwa; alitoa amri, nao ukajitokeza. Yawe anavunja mipango ya mataifa, na anabadilisha mawazo yao. Mipango ya Yawe inadumu milele; kusudi lake linadumu kwa vizazi vyote. Heri taifa ambalo Mungu wake ni Yawe; heri wale aliowachagua kuwa watu wake mwenyewe! Yawe anaangalia chini kutoka mbinguni, na kuwaona wanadamu wote. Kutoka kwenye kiti chake cha kifalme, anawaangalia wakaaji wote wa dunia. Yeye anaunda mioyo ya watu wote, yeye anajua kila kitu wanachofanya. Mufalme hawezi kuokolewa kwa kuwa na kundi kubwa; wala shujaa hapati ushindi kwa nguvu zake kubwa. Farasi wa vita hafai kitu kwa kupata ushindi; nguvu zake nyingi haziwezi kumwokoa mutu. Yawe anawaangalia wale wanaomwabudu, watu ambao wanatumainia wema wake. Yeye anawaokoa katika kifo, anawalinda wakati wa njaa. Mioyo yetu inamutumainia Yawe. Yeye ni musaidizi wetu na ngao yetu. Tunafurahi kwa sababu yake; tunatumainia jina lake takatifu. Wema wako ukae nasi, ee Yawe, kwa maana tumekuwekea tumaini letu. Kwa mukubwa wa waimbaji. Zaburi ya Daudi alipojifanya mwenda-wazimu mbele ya mufalme Abimeleki naye akamufukuza na Daudi akajiendea. Nitamutukuza Yawe nyakati zote, sitaacha hata kidogo kutaja sifa zake. Mimi nitajisifu kwa ajili ya Yawe; wanyenyekevu wasikie na kufurahi. Mumutukuze Yawe pamoja nami, wote pamoja tulisifu jina lake. Nilimwomba Yawe, naye akanijibu, na kuniondoa katika hofu zangu zote. Mumugeukie Mungu mupate kufurahi; nanyi hamutafezeheka hata kidogo. Masikini alimulilia Yawe, naye akamusikia, na kumwokoa katika taabu zake zote. Malaika wa Yawe anawalinda wote wanaomwabudu, na kuwaokoa kutoka katika hatari. Mupime muone jinsi Yawe ni muzuri. Heri mutu anayekimbilia kwake. Mumwabudu Yawe, enyi watakatifu wake, maana wenye kumwabudu hawakosewi kitu. Hata simba wakali wanakosewa na kusikia njaa, lakini wanaomutafuta Yawe hawakosewi chochote kizuri. Mukuje, enyi vijana munisikilize, nami nitawafundisha kumwabudu Yawe. Unatamani kufurahia maisha, kuishi maisha marefu na kufurahia mazuri? Basi, uache kusema mabaya, na kuepuka kusema uongo. Ujiepushe na uovu, utende mazuri; utafute amani na kuifuatilia. Yawe anawaangalia watu wa haki, na kusikiliza malalamiko yao; lakini anawapinga watu wanaotenda maovu, kusudi afute majina yao kutoka katika dunia. Watu wa haki wakimulilia Yawe, yeye anawasikia, na kuwaokoa katika taabu zao zote. Yawe ni karibu na wenye kuvunjika moyo; anawaokoa wote waliokata tamaa kabisa. Mateso ya mutu wa haki ni mengi, lakini Yawe anamwokoa kutoka katika yote. Analinda viungo vya mwili wake wote, hakuna hata mufupa wake mumoja utakaovunjwa. Ubaya unawaletea waovu kifo; wanaowachukia watu wa haki wataazibiwa. Yawe anaokoa maisha ya watumishi wake, wote wanaomukimbilia hawataazibiwa. Zaburi ya Daudi. Uwapinge, ee Yawe, hao wanaonipinga; uwashambulie hao wanaonishambulia. Utwae ngao yako na kikingio chako, uinuke ukuje kunisaidia! Chukua mukuki na upanga wako kwa kuwazuia wale wanaonifuata. Uniambie mimi kwamba utaniokoa. Wapate haya na kuzarauliwa, hao wanaotaka kupoteza maisha yangu! Warudishwe nyuma na kufezeheka, hao wanaonitafutia hasara. Wakuwe kama maganda yanayopeperushwa na upepo, wakikimbizwa na malaika wa Yawe! Njia yao ikuwe ya giza na utelezi, wakifukuzwa na malaika wa Yawe! Maana walinitegea mitego bila sababu; walinichimbia shimo bila neno lolote. Maangamizi yawapate wao kwa rafla, wanaswe katika mutego wao wenyewe, watumbukie katika shimo lao wenyewe! Hivi nitamufurahia Yawe; nitashangilia kwa sababu yeye ameniokoa. Nitamwambia Yawe kwa moyo wangu wote: “Wewe, ee Yawe, hakuna anayekuwa kama wewe! Wewe unawaokoa wamasikini kutoka makucha ya wenye nguvu, wamasikini na wakosefu kutoka mikono ya wanyanganyi.” Washuhuda wakorofi wanajitokeza, wananiuliza mambo nisiyoyajua. Wananilipa mabaya kwa mazuri; nami pekee nimebaki ukiwa. Lakini wao walipokuwa wagonjwa, mimi nilivaa magunia kuonyesha huzuni, nilijitesa kwa kufunga kula chakula. Niliomba nikikuwa nimeinamisha kichwa. Nikakuwa kama ninamulilia rafiki au ndugu yangu. Nilikwenda huku na huko kwa huzuni, kama mutu anayeomboleza kifo cha mama yake. Lakini mimi nilipoanguka, walikusanyika kunisimanga. Walikusanyika kuniuzi. Wageni nisiowajua walinizomea bila kukoma, wala hakuna aliyewazuia. Walinichekelea, walinisagia meno. Ee Yawe, utaangalia tu mpaka wakati gani? Uniokoe kutoka mashambulio yao; uokoe maisha yangu kutoka simba wakali hao. Hivi nitakushukuru kati ya kusanyiko kubwa la watu; nitakutukuza kati ya kundi kubwa la watu. Usiwaache waadui hao wabaya wanisimange, hao wanaonichukia bure, wafurahie mateso yangu. Hawasemi vizuri juu ya wengine, wanatunga tu uongo juu ya wanainchi watulivu. Wananishitaki kwa sauti, wakisema: “Sawa! Sawa! Tumeona wenyewe uliyotenda!” Lakini wewe Yawe unaona jambo hilo. Usinyamaze, ee Yawe, usikae mbali nami. Uinuke, ee Yawe, unitetee; ukuje, ee Mungu wangu, uangalie maneno yangu. Ee Yawe, Mungu wangu, unitetee, unitendee kulingana na haki yako. Usiwaache waadui zangu wanisimange. Usiwaache waseme: “Tumefanikiwa sawa tulivyotaka!” au waseme: “Tumemumaliza huyu!” Uwaache hao wanaofurahia hasara yangu, washindwe wote na kufezeheka. Hao wote wanaojiona bora kuliko mimi, wapate haya na kufezeheka. Lakini wanaotaka kuona kwamba sina kosa, wakuwe na furaha tele, waseme siku zote: “Yawe ni mukubwa! Anapendezwa na kumupatia mutumishi wake uheri.” Hivi nitatangaza haki yako; nitasema sifa zako muchana kutwa. Kwa mukubwa wa waimbaji. Zaburi ya Daudi, mutumishi wa Yawe. Zambi inaongea na mutu mwovu, ndani kabisa ya moyo wake; kuogopa Mungu si kitu kwake. Mwovu anajipendelea mwenyewe, anafikiri uovu wake hautagunduliwa na kulaaniwa. Kila anachosema ni uovu na uongo; ameacha kutumia hekima na kutenda mema. Anapolala anawaza kutenda maovu, anajiweka katika njia isiyokuwa nzuri, wala hachukii uovu. Wema wako, ee Yawe, unaenea hata mbinguni; uaminifu wako unafika hata kwenye mawingu. Haki yako ni kama milima mikubwa, hukumu zako ni kama vilindi vya bahari. Wewe, ee Yawe, unawalinda wanadamu na nyama. Kweli wema wako ni bora! Wanadamu wanakimbilia kwenye kivuli cha mabawa yako. Unawashibisha kwa utajiri wa nyumba yako; unawakunywesha katika muto wa wema wako. Wewe ndiwe asili ya uzima; kwa mwangaza wako tunaona mwangaza. Uendelee kuwatendea mema wale wanaokutambua; uzidi kuokoa wenye moyo wenye kunyooka. Usikubali wenye majivuno wanishambulie, wala watu waovu wanikimbize. Kumbe watenda maovu wameanguka; wameangushwa chini, hawawezi kuinuka. Zaburi ya Daudi. Usihangaike kwa sababu ya waovu; usiwaonee wivu wanaotenda mabaya. Maana hao watatoweka mara moja kama nyasi; watanyauka kama majani. Umutumainie Yawe na kutenda mazuri, upate kuishi katika inchi na kuwa salama. Uitafute furaha yako kwa Yawe, naye atakujalia unayotamani katika moyo. Umutolee Yawe maisha yako, umutumainie yeye, naye atakufanyia kitu. Ataifanya haki yako iangae kama mwangaza wa jua muchana kati. Tulia mbele ya Yawe, umungojee kwa uvumilivu; usihangaike juu ya wale wanaofanikiwa, ndio watu wanaojaliwa katika mipango yao mibaya. Usiwake hasira wala kuwa na kasirani; usihangaike, maana hiyo inazidisha ubaya. Watu wanaotenda mabaya wataangamizwa, lakini wanaomutumainia Yawe watarizi inchi. Bado kidogo, mwovu atatoweka; utamutafuta pale alipokuwa, wala hautamwona. Lakini wapole watarizi inchi, hao wataifurahia amani kamili. Mwovu anamufanyia mutu wa haki shauri baya, na kumusagia meno kwa chuki. Lakini Yawe anamuchekelea mwovu, kwa maana anajua mwisho wake ni karibu. Waovu wanachomoa panga na kuvuta pinde zao, wapate kuwaua wamasikini na wakosefu; wawachinje watu wenye mwenendo sawa. Lakini panga zao wenyewe zitawapenya mioyo, na pinde zao zitavunjwavunjwa. Afazali mali kidogo ya mutu wa haki kuliko utajiri mwingi wa watu waovu. Maana nguvu za waovu zitavunjwa, lakini Yawe atawaimarisha watu wa haki. Yawe anatunza maisha ya watu wakamilifu, na urizi wao utadumu milele. Hawatafezeheka nyakati mbaya zikiwafikia; siku za njaa watakuwa na chakula tele. Lakini waovu wataangamia, waadui za Yawe watanyauka kama maua katika jangwa; kweli watatoweka kama moshi. Mutu mwovu anakopesha bila kurudisha; lakini mutu wa haki anatoa kwa moyo safi. Waliobarikiwa na Yawe watarizi inchi, lakini waliolaaniwa naye wataongolewa. Yawe anaongoza mutu katika njia yake, anamulinda yule anayemupendeza. Hata akianguka, hatabaki chini, kwa sababu Yawe anamuimarisha. Nilikuwa kijana na sasa mimi ni muzee; hata kidogo sijaona mutu wa haki ameachwa na Mungu, au watoto wake wakiombaomba chakula. Siku zote yeye anakopesha kwa moyo safi, na watoto wake ni wenye baraka. Achana na uovu, utende mazuri, nawe utaishi katika inchi siku zote; maana Yawe anapenda haki, wala hawaachi waaminifu wake. Anawalinda hata milele; lakini wazao wa waovu wataangamizwa. Watu wa haki watarizi inchi, nao wataishi humo milele. Mutu wa haki anasema maneno ya hekima, kwa ulimi wake anasema kufuatana na sheria ya Mungu. Sheria ya Mungu wake ni ndani ya moyo wake, naye hapiti pembeni katika mwenendo wake. Mutu mwovu anamuvizia mutu wa haki, na kujaribu kumwua; lakini Yawe hatamutoa mutu wa haki katika makucha yake, wala kumwachilia aazibiwe anaposhitakiwa. Umutumainie Yawe na kushika njia yake, naye atakuinua uirizi inchi, na kuwaona waovu wakiongolewa. Nilimwona mwovu aliyejivuna sana, akinyanyua shingo juu kama mierezi ya Lebanoni! Kisha nikapita pale, naye hakukuwa tena; nikamutafuta, lakini hakuonekana tena. Muangalie mutu mukamilifu, mutu wa usawa; mutu anayependa amani anajaliwa wazao. Lakini wakosaji wote wataangamizwa; na wazao wao wataongolewa. Yawe anawaokoa watu wa haki, na kuwalinda wakati wa taabu. Yawe anawasaidia na kuwaokoa; anawaopoa kutoka makucha ya waovu na kuwaokoa, maana wanakimbilia kwake. Zaburi ya Daudi, inayoelekea sadaka yake ya ukumbusho. Ee Yawe, usiniazibu kwa hasira yako, usiniadibishe kwa kasirani yako. Mishale yako imenichoma; mukono wako umenigandamiza. Hakuna uzima katika mwili wangu, kwa sababu umenikasirikia. Hakuna afya hata katika mifupa yangu, kwa sababu ya zambi yangu. Nimefunikwa kabisa na zambi zangu, zinanilemea kama muzigo muzito sana. Vidonda vyangu vimeoza na kunuka, na hayo ni matokeo ya ujinga wangu. Nimepinduka mpaka chini na kupondekana; muchana kutwa ninazunguka nikiomboleza. Viungo vyangu vimeshambuliwa na homa; hakuna uzima katika mwili wangu. Nimeregea na kupondekanapondekana; ninaugua kwa kusongwa katika moyo. Yawe, wewe unajua mahitaji yangu yote; sifichi kilio changu mbele yako. Moyo wangu unapigapiga, nguvu zimeniishia; hata macho yangu nayo yamekwisha fifia. Warafiki na wenzangu wanaepuka kuona mateso yangu, na wandugu zangu wanakaa mbali nami. Wanaotaka kuniua wanatega mitego yao; wanaonitakia niumie wanakusudia kuniangamiza. Muchana kutwa wanafanya mipango juu yangu. Lakini mimi nimekuwa kama kiziwi, sisikii; nimekuwa kama bubu asiyeweza kusema kitu. Kweli, nimekuwa kama mutu asiyesikia, kama mutu asiyekuwa na chochote cha kujitetea. Lakini ninakutumainia wewe, ee Yawe; wewe, ee Yawe, Mungu wangu, ndiwe utakayenijibu. Ninakuomba tu waadui wasinisimange, wasijitukuze juu ya kuanguka kwangu. Mimi ni karibu ya kuanguka; ninakuwa na maumivu ya siku zote. Ninaungama uovu wangu; zambi zangu zinanisikitisha. Waadui zangu ni wazima, wana nguvu, ni wengi sana hao wanaonichukia bure. Hao wanaonilipa mabaya kwa mazuri, wananipinga kwa sababu ninatenda mazuri. Usinitupe, ee Yawe; ee Mungu wangu, usikae mbali nami. Ukuje haraka kunisaidia, ewe Yawe, mwokozi wangu. Kwa mukubwa wa waimbaji. Kwa mutindo wa Yedutuni. Zaburi ya Daudi. Nilisema: “Nitayachunga maisha yangu, kusudi nisitende zambi kwa usemi wangu. Nitafunga midomo yangu waovu wanapokuwa karibu nami.” Nilikuwa kama bubu, bila kusema kitu, nilinyamaza lakini sikupata faida. Mateso yangu yalizidi kuwa makali, mahangaiko yangu yakaniunguza katika moyo. Kadiri nilivyowaza ndivyo nilivyotaabika, kisha maneno haya yakanitoka: “Ee Yawe, unijulishe mwisho wangu, siku zangu za kuishi zimenibakia ngapi, nijue namna maisha yangu yanavyopita upesi!” Kumbe umenipimia maisha mafupi sana! Maisha yangu si kitu mbele yako. Hakika, kila mwanadamu ni kama pumzi tu! Kweli, kila mutu anapita kama kivuli; masumbuko yake yote ni bure tu; anakusanya mali, hajui atakayeipata! Na sasa, ee Bwana, ninatazamia nini? Tumaini langu ni kwako wewe! Uniokoe katika makosa yangu yote; usikubali wapumbafu wanichekelee. Niko kama bubu, sisemi kitu, kwa maana wewe ndiwe uliyetenda hayo. Usiniazibu tena; ninamalizika kwa mapigo yako. Unapomwazibu mutu zambi zake kwa kumwadibisha, unaharibu kama nondo kile anachokipenda. Hakika, kila mwanadamu ni kama pumzi tu! Usikie maombi yangu, ee Yawe, usikilize kilio changu, usikae kimya ninapolia. Maana, mimi ni kama mugeni tu anayepita, ni musafiri kama vile babu zangu wote walivyokuwa. Uache kuniangalia nipate kufurahi kidogo, mbele sijaaga dunia na kutoweka kabisa. Kwa mukubwa wa waimbaji. Zaburi ya Daudi. Nilimungojea Yawe kwa uvumilivu, akanielekea na kusikia kilio changu. Aliniondoa katika shimo la hatari, alinitoa katika matope mengi, akanisimamisha salama juu ya mulima, na kuziimarisha hatua zangu. Alinifundisha wimbo mupya, wimbo wa sifa kwa Mungu wetu. Wengi wataona, wataogopa, na kisha watamutumainia Yawe. Heri mutu anayemutumainia Yawe, mutu asiyejiunga na watu wenye majivuno, watu waliopotoka kwa kuabudu miungu ya uongo. Ee Yawe, Mungu wangu, umetufanyia maajabu mengi, na mipango yako juu yetu haihesabiki; hakuna yeyote anayekuwa kama wewe. Kama ningeweza kusimulia hayo yote, hesabu yake ingenishinda. Wewe hautaki sadaka za kuteketezwa kwa moto wala matoleo, sadaka za nyama za kuteketezwa wala za kusamehewa zambi, lakini umenipa masikio nikusikie. Halafu nikasema: “Ninakuja. Katika kitabu imeandikwa juu yangu. Ninataka kutimiza mapenzi yako, ee Mungu wangu; sheria yako ninaishika kwa moyo wangu wote!” Nimesimulia habari njema ya ukombozi, mbele ya kusanyiko kubwa la watu. Kama unavyojua, ee Yawe, mimi sikujizuia kuitangaza. Sikuficha katika moyo wangu ukombozi ulionijalia. Nimetangaza siku zote kwamba wewe ni mwokozi mwaminifu. Sikuficha kusanyiko kubwa la watu wema wako na uaminifu wako. Ee Yawe, usikose kunirehemu! Wema na uaminifu wako vinilinde. Hatari zisizohesabika zinanizunguka, maovu yangu yananisonga hata siwezi kuona; ni mengi kuliko nywele zangu, nami nimevunjika moyo. Upendezwe, ee Yawe, kuniokoa; ee Yawe, ukuje haraka kunisaidia. Wote wanaokusudia kuniangamiza, wafezeheke pamoja! Hao wanaotamani niumie, warudi nyuma na kuzarauliwa! Hao wanaonisimanga, wafezeheke kwa kushindwa kwao! Lakini wanaokutafuta wafurahi na kushangilia. Wanaopenda uwaokoe waseme siku zote: “Yawe ni mukubwa!” Mimi ni masikini na mukosefu, ee Bwana; lakini wewe haukunisahau. Wewe ni musaada wangu na mwokozi wangu; ukuje, ee Mungu wangu, usikawie! Kwa mukubwa wa waimbaji. Zaburi ya Daudi. Heri mutu anayeshugulikia masikini; Yawe atamwokoa wakati wa shida. Yawe atamulinda na kuchunga uzima wake, naye atafanikiwa katika inchi; hatamwacha katika makucha ya waadui zake. Yawe atamusaidia anapokuwa mugonjwa, atamuponyesha magonjwa yake yote. Nami nilisema: “Unirehemu, ee Yawe, uniponyeshe, maana nimekukosea.” Waadui zangu wanasema hivi vibaya juu yangu: “Atakufa wakati gani kusudi jina lake lisahauliwe!” Wananitembelea bila kuwa na nia njema, wanawaza mabaya juu yangu, wanapofika inje wanawatangazia wengine. Wote wanaonichukia wananongoneza juu yangu; wananiwazia mambo mabaya. Wanasema: “Magonjwa haya yatamwua; hatatoka tena ndani ya kitanda chake!” Hata rafiki yangu wa moyo niliyemwamini, rafiki aliyechangia chakula nami, amegeuka kunishambulia! Ee Yawe, unionee huruma! Uniponyeshe, nami nitawalipiza kisasi. Hivyo nitajua kwamba unapendezwa nami, waadui zangu wasipopata ushindi juu yangu. Wewe unaniimarisha katika ukamilifu; utanichunga mbele yako milele. Yawe, Mungu wa Israeli, asifiwe, tangu milele na hata milele! Amina! Amina! Kwa mukubwa wa waimbaji. Mashairi ya Wakora. Kama pongo anavyotamani maji ya kijito, ndivyo ninavyokutamani, ee Mungu wangu! Ninasikia kiu ya Mungu, kiu ya Mungu Mwenye Uzima. Nitafika kwake wakati gani na kuuona uso wake? Machozi ni chakula changu muchana na usiku; ninaambiwa kila siku: “Mungu wako yuko wapi?” Katika huzuni yangu, ninakumbuka jinsi nilivyokwenda na kundi la watu na kuwaongoza kwenda katika nyumba ya Mungu wakipiga vigelegele vya shukrani, kundi la watu likifanya sherehe! Mbona ninaugua hivyo katika moyo? Kwa nini ninahangaika hivyo ndani yangu? Nitamutumainia Mungu, maana nitamusifu tena yeye anayekuwa musaada wangu na Mungu wangu. Roho yangu imeregea kabisa, kwa hiyo ninakukumbuka wewe, ee Mungu, kutoka katika eneo la Yordani, kutoka mulima Hermoni na Mizari. Mafuriko juu ya mafuriko yananguruma, mawimbi na zoruba yako vinanifunika. Yawe atanijalia wema wake muchana; nami nitamwimbia wimbo wa sifa usiku, nitamwomba Mungu anayenipa uzima. Ninamwambia Mungu, yeye kikingio changu: “Kwa nini umenisahau? Kwa nini niende huko na huko nikiomboleza kwa kuteswa na adui yangu?” Nimepondekana kwa ajili ya matukano yao, wanaponiuliza kila siku: “Mungu wako, yupo wapi?” Mbona ninaugua hivyo katika moyo? Kwa nini ninahangaika hivyo ndani yangu? Nitamutumainia Mungu, maana nitamusifu tena Mungu, anayekuwa musaada wangu na Mungu wangu. Unipatie haki yangu, ee Mungu; uyatetee maneno yangu mbele ya watu wabaya; uniokoe na watu waongo na waovu. Ninakimbilia kwako, ee Mungu; kwa nini umenitupilia mbali? Kwa nini niende huko na huko nikiomboleza kwa kuteswa na adui yangu? Utumie mwangaza na ukweli wako viniongoze, vinipeleke kwenye mulima wako mutakatifu, kwenye makao yako. Hapo, ee Mungu, nitakwenda kwenye mazabahu yako; nitakuja kwako, ee Mungu, wewe furaha yangu kubwa. Nitakusifu kwa zeze, ee Mungu, Mungu wangu. Mbona ninahuzunika hivyo katika moyo? Kwa nini ninahangaika hivyo ndani mwangu? Nitamutumainia Mungu, nitamusifu tena yeye anayekuwa musaada wangu na Mungu wangu. Kwa mukubwa wa waimbaji. Mashairi ya Wakora. Ee Mungu, sisi tumesikia kwa masikio yetu, babu zetu wametuelezea mambo uliyotenda nyakati zao, ndiyo mambo uliyotenda hapo kale. Kwa mukono wako mwenyewe uliyafukuza mataifa, na mahali pao ukawaikalisha watu wako; uliyaazibu mataifa, na kuwafanikisha watu wako. Watu wako hawakuitwaa inchi kwa silaha zao, wala hawakupata ushindi kwa nguvu zao, lakini kwa mukono wako mwenyewe, kwa kuwaangazia uso wako, maana wewe uliwapenda. Wewe ni mufalme wangu na Mungu wangu! Unawajalia ushindi wazao wa Yakobo. Kwa nguvu yako tunawashinda waadui zetu, kwa jina lako tunawakanyaga wanaotushambulia. Mimi sitegemei upinde wangu, wala upanga wangu hauwezi kuniokoa. Wewe ndiwe uliyetuokoa kutoka waadui zetu; uliwavuruga wale waliotuchukia. Siku zote tunakutukuza, ee Mungu; tutakutolea shukrani kwa milele. Lakini sasa umetuacha na kutufezehesha; hauendi tena na makundi yetu ya waaskari. Umetufanya tuwakimbie waadui zetu, nao wakanyanganya mali zetu. Umetufanya kama kondoo wanaopelekwa kuchinjwa; umetutawanya kati ya mataifa. Umeuzisha watu wako kwa bei ya chini; wala haukupata faida yoyote. Umetupotezea heshima mbele ya jirani zetu, nao wanatuchekelea na kutuzarau. Umetufanya tuzarauliwe na watu wa mataifa; wanatutikisia vichwa vyao kwa kutusimanga. Muchana kutwa nimefezeheka, na uso wangu umejaa haya tele kwa ajili ya maneno na mazarau ya wenye kunitukana, kwa ajili ya waadui zangu wenye kunilipiza kisasi. Hayo yote yametupata sisi ijapokuwa hatujakusahau, wala hatujavunja agano lako. Hatujakuasi wewe, wala hatujaiacha njia yako. Hata hivyo umetupondaponda kati ya nyama wakali; umetuacha katika giza nzito sana. Tungalikuwa tumekusahau wewe Mungu wetu, na kumukimbilia mungu wa uongo, ee Mungu, ungalikwisha jua jambo hilo, kwa maana wewe unajua siri za moyo. Lakini kwa ajili yako tunauawa kila siku; tunatendewa kama kondoo wa kuchinjwa. Amuka, ee Bwana! Mbona umelala? Inuka! Tafazali usitutupe milele! Mbona unajificha mbali nasi, na kusahau taabu na mateso yetu? Tumeinama mpaka katika mavumbi, tumebanana na udongo. Uinuke, ukuje kutusaidia! Utukomboe kwa sababu ya wema wako. Kwa mukubwa wa waimbaji. Kwa mutindo wa wimbo: “Mayungiyungi.” Mashairi ya Wakora. Wimbo wa mapenzi. Moyo wangu umejaa mawazo mazuri: ninamutungia mufalme mashairi yangu, ulimi wangu ni kama kalamu ya mwandishi hodari. Wewe ni muzuri kuliko wanadamu wote, maneno yako ni rehema tupu, Mungu amekubariki milele. Ujifungie upanga wako, ewe shujaa! Wewe ni mutukufu na mwenye mamlaka. Songa mbele kwa utukufu upate ushindi, utetee ukweli na kulinda haki. Mukono wako utende mambo makubwa. Mishale yako ni mikali, inapenya mioyo ya waadui za mufalme; nayo mataifa yanaanguka chini yako. Kiti chako cha kifalme ni imara, kinadumu milele kama cha Mungu. Wewe unatawala watu wako kwa haki. Unapenda haki na kuchukia uovu. Kwa hiyo Mungu, Mungu wako, amekupendelea kuliko wenzako; amekuweka kuwa mufalme kwa kukupakaa mafuta ya kufurahisha. Nguo zako zinanuka marasi, udi, na mudalasini; muziki wa vinubi unakufurahisha katika nyumba ya pembe za tembo. Wabinti za wafalme ni kati ya wanaokupokea, naye malkia amesimama kwa kuume kwako, amevaa mapambo ya zahabu safi kabisa ya Ofiri. Sikiliza binti, ufikiri! Tega sikio lako: sahau sasa taifa lako na jamaa yako. Uzuri wako unavuta moyo wa mufalme; yeye ni bwana yako, lazima umutii. Watu wa Tiro watakuletea zawadi; watajiri watajipendekeza kwako. Binti wa mufalme anaingia, naye ni muzuri kabisa! Nguo yake imefumwa na nyuzi za zahabu. Akiwa amevaa nguo za rangi nyingi, anaongozwa kwa mufalme, akisindikizwa na wabinti wenzake. Kwa furaha na shangwe wanafika huko, na kuingia katika nyumba ya mufalme. Ee mufalme, utapata watoto wengi watakaotawala pahali pa babu zako; utawafanya watawale katika dunia yote. Nitalifanya jina lako litukuzwe katika vizazi vyote, nayo mataifa yatakusifu milele. Kwa mukubwa wa waimbaji. Zaburi ya Wakora: Kwa mutindo wa Sauti ya juu kabisa. Mungu ni kimbilio letu na nguvu yetu; yeye ni musaada wetu wakati wa taabu. Kwa hiyo hatutaogopa kitu chochote, hata dunia ikiyeyuka na milima kutikisika kutoka bahari, hata kama bahari ikichafuka na kutisha, na milima ikitetemeka kwa machafuko yake. Kuna muto ambao maji yake yanafurahisha muji wa Mungu, makao matakatifu ya Mungu Mukubwa. Mungu yuko katika muji huo, nao hauwezi kutikiswa; Mungu ataupatia musaada kila asubui. Mataifa yanakasirika na falme zinatikisika; Mungu ananguruma, nayo dunia inayeyuka. Yawe wa majeshi yuko pamoja nasi, Mungu wa Yakobo ni kimbilio letu. Mukuje muone matendo ya Yawe. Muone maajabu aliyofanya katika dunia. Anakomesha vita popote katika dunia. Anavunjavunja pinde na mikuki, nayo magari ya vita anayateketeza. Anasema: “Munyamaze na kujua kwamba mimi ni Mungu! Mimi ninatukuzwa katika mataifa yote; mimi ninatukuzwa katika ulimwengu wote!” Yawe wa majeshi yuko pamoja nasi, Mungu wa Yakobo ni kimbilio letu. Kutoka Mukubwa wa Wakora. Zaburi ya Wakora. Enyi watu wote, mupige vigelegele! Mumusifu Mungu kwa sauti za shangwe! Maana Yawe, Mungu Mukubwa, anaogopesha. Yeye ni mufalme mukubwa wa ulimwengu wote. Ametuwezesha kuwashinda watu wa mataifa, ameyaweka mataifa chini ya mamlaka yetu. Ametuchagulia inchi hii ikuwe urizi wetu, ambayo ni utukufu wa Yakobo anayemupenda. Mungu anapanda kwenye kiti chake cha kifalme, anashangiliwa na kupigiwa baragumu. Mumwimbie Mungu sifa, mumwimbie! Mumwimbie mufalme wetu sifa, mumwimbie! Mumwimbie Mungu mashairi ya sifa; maana yeye ni mufalme wa ulimwengu wote. Mungu anatawala mataifa yote; ameikaa katika kiti chake kitakatifu cha kifalme. Waongozi wa mataifa wanakusanyika, wanajiunga na watu wa Mungu wa Abrahamu, maana watawala wa dunia wako chini ya Mungu, yeye ni juu ya yote. Zaburi ya Wakora. Yawe, ni mukubwa; anastahili kusifiwa sana katika muji wake, ndio mulima wake mutakatifu. Sayuni, mulima wa Mungu, unapendeza kwa urefu; muji wa Mufalme mukubwa ni furaha ya ulimwengu. Mungu analinda pango zake za kukimbilia; yeye anajulikana kuwa upango wake. Wafalme walikusanyika, wakaenda pamoja kushambulia. Lakini walipouona Sayuni, wakashangaa; wakashikwa na hofu na kukimbia. Hofu kubwa iliwashika, wakasikia uchungu kama mama anayezaa, kama vile wenye kurushwa na upepo mukali wa mashariki, ambao unavunjavunja mashua kubwa sana za Tarsisi. Yote tuliyosikia tumejionea wenyewe katika muji wa Yawe wa majeshi, katika muji wa Mungu wetu: Mungu atauimarisha milele. Ee Mungu, tunakumbuka wema wako tunapokuwa katika hekalu lako. Jina lako linasifiwa kila pahali, sifa zako zinaenea fasi zote katika dunia. Kwa mukono wako umetenda kwa haki. Watu wa Sayuni wafurahi! Watu wa Yuda washangilie, kwa sababu ya hukumu yako ya haki! Mutembee huko Sayuni, muuzunguke, muihesabu minara yake. Muangalie kuta zake na kuchunguza pango zake za kukimbilia, mupate kuelezea vizazi vitakavyokuja kwamba: “Huyu ni Mungu, Mungu wetu milele! Atakuwa mwongozi wetu milele!” Kwa mukubwa wa waimbaji. Zaburi ya Wakora. Musikie jambo hili, enyi watu wote! Mutege masikio, enyi wakaaji wote wa dunia. Musikilize wote, wakubwa na wadogo, enyi watajiri na wakosefu. Maneno yangu ni mazitomazito; mawazo yangu ni ya hekima. Ninatega sikio, nisikilize mezali, ninafafanua kitendawili kwa muziki wa zeze. Kwa nini niogope wakati wa hatari, wakati ninapozungukwa na uovu wa waadui? Watu waovu wanategemea mali zao, wanajisifia wingi wa utajiri wao. Lakini mwanadamu hawezi hata kidogo kujikomboa mwenyewe; hawezi kumulipa Mungu bei ya maisha yake, maana malipo ya ukombozi wa maisha ni kubwa sana. Hawezi kutoa kitu chochote kinachotosha, kimwezeshe aendelee kuishi siku zote, bila kuona kaburi. Inaonekana wazi kuwa hata wenye hekima wanakufa, nao wapumbafu na wajinga vilevile. Wote wanawaachia wengine mali zao. Ingawa walisema kwamba udongo ni wao, lakini ni makaburi ndiyo nyumba zao hata milele, ni makao yao vizazi hata vizazi. Mwanadamu hadumu katika utajiri wake; anakufa tu kama nyama. Hayo ndiyo yanayowapata wanaojitumainia kwa upumbafu, ndio mwisho wa wale wanaojivunia mali zao. Wanaongozwa kama kondoo mpaka katika kuzimu; kifo ndiye muchungaji wao. Wanashuka moja kwa moja katika kaburi. Miili yao inaozea huko. Kuzimu inakuwa makao yao. Lakini Mungu atanikomboa kutoka katika kuzimu, ataniopoa kutoka huko. Usihangaike ukiona mutu anatajirika, wala mali yake ikiongezeka zaidi na zaidi. Maana atakapokufa hatachukua kitu chochote, mali yake haitashuka huko chini pamoja naye. Hata akijitukuza katika maisha haya, na kusifiwa kwa sababu ya kufanikiwa, atakwenda kukutana na babu zake waliomutangulia kufa, ambao hawawezi kuona tena mwangaza. Mwanadamu hadumu katika utajiri wake: anakufa tu kama nyama. Zaburi ya Asafu. Mungu, Mungu Yawe, amesema, amewaita wakaaji wa dunia, tokea magaribi mpaka mashariki. Kutoka Sayuni, muji muzuri kupita kipimo, Mungu anajitokeza, akiangaza. Mungu wetu anakuja, lakini si kimyakimya: moto wenye kuteketeza unamutangulia, na zoruba kali inamuzunguka. Kutoka juu anaita mbingu na dunia kuwa washuhuda wake atakapowahukumu watu wake. Yeye anasema: “Munikusanyie waaminifu wangu, waliofanya agano nami kwa njia ya sadaka!” Mbingu zinatangaza haki ya Mungu; Mungu mwenyewe ndiye mwamuzi. “Enyi watu wangu, munisikilize, mimi Mungu, Mungu wenu! Ninataka kusema nanyi. Israeli, ninakuonya. Sikukaripii kwa sababu ya sadaka zako; haujaacha kunitolea sadaka za kuteketezwa. Kwa kweli sihitaji ngombe dume wa zizi lako, wala beberu wa nyumba yako, maana nyama wote wa pori ni mali yangu, na maelfu ya nyama wa milima ni wangu. Ndege wote wa mwitu ni mali yangu, na viumbe vyote vinavyoishi katika pori ni vyangu. Kama ningesikia njaa, singekuambia wewe, maana ulimwengu na vyote vinavyokuwa ndani yake ni vyangu. Unazani ninakula nyama ya ngombe dume, au kunywa damu ya mbuzi? Shukrani ikuwe ndiyo sadaka yako kwa Mungu. Umutimizie Mungu Mukubwa ahadi zako. Uniite wakati wa taabu, nami nitakuokoa, nawe utanitukuza.” Lakini Mungu anamwambia mutu mwovu: “Kwa nini kutajataja tu masharti yangu? Kwa nini unasemasema juu ya agano langu? Wewe unachukia maonyo, na maneno yangu haupendi kuyafuata. Ukimwona mwizi, unajiunga naye, nawe unashirikiana na washerati. Uko tayari siku zote kusema mabaya; kazi ya ulimi wako ni kutunga uongo. Unaikaa kitako kumuteta mwanadamu mwenzako, unamuchongea ndugu yako wa tumbo. Umefanya hayo yote nami nimenyamaza. Unazani kwamba mimi ni kama wewe? Lakini sasa nitakukaripia, nitakugombeza waziwazi. “Mufikiri vizuri jambo hili, enyi musionijali, kama sivyo nitawaangamiza, wala hakuna atakayewaokoa. Anayenitolea shukrani kama sadaka yake, huyo ndiye anayenitukuza; yeyote anayedumu katika njia yangu, huyo ndiye nitakayemwokoa.” Unihurumie, ee Mungu, kadiri ya wema wako; uyafute makosa yangu, kadiri ya wingi wa rehema yako. Unisafishe kabisa kosa langu; unitakase zambi yangu. Ninaitikia kabisa makosa yangu, siku zote ninaona waziwazi zambi yangu. Nimekukosea wewe peke yako, nimetenda mabaya mbele yako. Hivi uamuzi wako ni wa haki, hukumu yako haipotoki. Mimi ni mukosaji tangia kuzaliwa kwangu, mwenye zambi tangia tumbo la mama yangu. Wewe unataka moyo wa ukweli; hivyo unifundishe kuwa na moyo wa hekima. Unitakase kwa hisopo, nikuwe safi, unisafishe, nikuwe mweupe pee. Unijaze furaha na shangwe, unifurahishe tena, mimi ambaye uliniponda. Ugeuke, usiangalie zambi zangu; uyafute makosa yangu yote. Ee Mungu, uniumbie moyo safi, uweke ndani yangu roho mupya na inayoimarika. Usinitupe mbali nawe; usiondoe roho yako takatifu ndani yangu. Unirudishie furaha ya wokovu wako, uniimarishe kwa Roho wako mwema. Halafu nitawafundisha wakosaji njia zako, nao wenye zambi watarudi kwako. Uniokoe kutoka kosa la kumwanga damu, ee Mungu, Mungu mwokozi wangu, nami nitaimba kwa sauti kwamba umeniokoa. Ee Bwana, uniwezeshe kusema, midomo yangu itangaze sifa zako. Kweli wewe haupendezwi na sadaka. Hautaki nikutolee sadaka za kuteketezwa. Sadaka ninayokutolea, ee Mungu, ni roho munyenyekevu. Haukatai moyo munyenyekevu na wa kutubu. Ee Mungu, upendezwe na kuutendea mazuri Sayuni; uzijenge tena upya kuta za Yerusalema. Halafu utapendezwa na sadaka za haki: ndizo sadaka za kuteketezwa na za kuteketezwa nzima. Ngombe dume watatolewa juu ya mazabahu yako. Mbona, ewe jitu, unajivunia mabaya unayotendea waaminifu. Kila wakati unawaza maangamizi. Ulimi wako ni kama wembe mukali. Unafikiria tu kutenda mabaya. Wewe unapenda ubaya kuliko uzuri, unapenda uongo kuliko ukweli. Ewe mudanganyifu mukubwa, unapenda mambo ya kuangamiza wengine. Kwa hiyo Mungu atakuangamiza milele, atakunyanyua na kukuondoa katika nyumba yako; atakuongoa katika inchi ya wenye kuishi. Watu wa haki wataona, wataogopa, na kisha watakuchekelea na kusema: “Muangalie yaliyomupata mutu huyu! Yeye hakutaka Mungu akuwe kimbilio lake, lakini alitegemea wingi wa mali yake, na kutafuta humo usalama wake!” Lakini mimi ni kama muzeituni mubichi, unaostawi katika nyumba ya Mungu. Ninategemea wema wake milele na milele. Ee Mungu, nitakushukuru siku zote, kwa ajili ya mambo uliyofanya. Nitatangaza kwamba wewe ni muzuri, mbele ya watu wako waaminifu. Kwa mukubwa wa waimbaji. Kwa mutindo wa wimbo wa huzuni. Mashairi ya Daudi. Mupumbafu anajisemesha hivi katika moyo: “Hakuna Mungu!” Wote wamepotoka kabisa, wametenda mambo ya kuchukiza; hakuna hata mumoja anayetenda mazuri. Mungu anawaangalia wanadamu kutoka mbinguni, aone kama kuna yeyote mwenye akili kama kuna yeyote anayemutafuta Mungu. Lakini wote wamekosa, wote wamepotoka pamoja; hakuna anayetenda mazuri, hakuna hata mumoja. Hao wanaotenda maovu hawajui kitu? Wanatafuna watu wangu kama mikate; wala hawajali Mungu. Hapo watashikwa na hofu, hofu ambayo hawajapata kuiona; maana Mungu ataitawanya mifupa ya waadui, hao watafezeheka maana Mungu amewakataa. Heri ukombozi wa Israeli ungefika kutoka Sayuni! Mungu atakapotengeneza hali ya watu wake, wazao wa Yakobo watashangilia; watu wa Israeli watafurahi. Ee Mungu, uniokoe kwa jina lako, unitetee kwa nguvu zako. Ee Mungu, usikilize maombi yangu; uyategee sikio maneno ya kinywa changu. Watu wenye kiburi wananishambulia, watu wakali wanawinda maisha yangu, watu ambao hawamujali Mungu. Ninajua Mungu ni musaada wangu, Yawe anaimarisha maisha yangu. Yeye atawaazibu waadui zangu kwa uovu wao wenyewe; kwa uaminifu wako, ee Mungu, uwaangamize. Nitakutolea sadaka kwa moyo wa furaha; nitalisifu jina lako maana wewe ni muzuri. Umeniokoa katika taabu zangu zote, nami nimewaona waadui zangu wameshindwa. Kutoka kwa mukubwa wa waimbaji: kwa vyombo vyenye nyuzi. Mashairi ya Daudi. Ee Mungu, tega sikio usikie maombi yangu; usiangalie pembeni ninapokuomba. Unisikilize na kunijibu; nimechoka na malalamiko yangu. Nina hofu kwa ajili ya vitisho vya waadui zangu, na kwa kuteswa na watu waovu. Watu waovu wananitaabisha, kwa hasira wananishambulia. Moyo wangu umejaa hofu, vitisho vya kifo vimenisonga. Ninatetemeka kwa hofu kubwa, nimeshikwa na vitisho vikubwa. Ninasema hivi: “Heri ningekuwa na mabawa kama njiwa! Ningeruka mbali na kupata pumziko, ningesafiri mbali sana, ningepata makao katika jangwa, ningekimbilia pahali penye usalama, mbali na upepo mukali na zoruba.” Ee Bwana, uwaangamize na kuvuruga luga yao, maana ninaona mateso ya ukali na ugomvi katika muji, vikiuzunguka muchana na usiku, na kuujaza hasara na ukorofi. Uharibifu umeenea popote katika muji, maovu na mapotovu kila pahali. Kama adui yangu angenitukana, ningeweza kuvumilia hayo; kama mupinzani wangu angenizarau, ningeweza kujificha mbali naye. Lakini, kumbe ni wewe mwenzangu; ni wewe rafiki yangu wa kweli! Sisi tulizoea kuzungumuza kirafiki; pamoja tulikwenda katika nyumba ya Mungu. Acha kifo kiwashitukie waadui zangu, washuke chini katika kuzimu wangali wazima; maana uovu umejaa katika mioyo yao. Lakini mimi ninamulilia Mungu, naye Yawe ataniokoa. Magaribi, asubui na muchana kati, ninalalamika na kulia, naye atasikia sauti yangu. Atanikomboa katika vita na kunipa amani, kwa maana waadui zangu ni wengi. Mungu anayetawala tangu milele, atanisikia na kuwafezehesha waadui yangu, maana hawapendi kubadilika, wala hawamwogopi Mungu. Mwenzangu amemushambulia rafiki yake, amevunja mapatano yake. Maneno yake ni matamu kuliko maziwa, lakini mawazo yake ni ya kufanya vita. Maneno yake ni laini kama mafuta, lakini yanakata kama upanga mukali. Utue muzigo wako kwa Yawe, naye atakusaidia; hamwachilii mutu wa haki ashindwe. Wewe, ee Mungu, utawaporomosha katika shimo chini kabisa. Wauaji na wadanganyifu hawatafikia nusu ya maisha yao. Lakini mimi nitakutumainia wewe, ee Mungu! Kwa mukubwa wa waimbaji. Kwa mutindo wa njiwa anayekaa mbali kwenye ukimya. Mashairi ya Daudi nyuma ya kukamatwa na Wafilistini kule Gati. Ee Mungu, unionee huruma, maana watu wananishambulia. Muchana kutwa waadui wananitesa. Muchana kutwa waadui zangu wananishambulia; ni wengi sana hao wanaonipiga vita. Ee Mungu Mukubwa, wakati ninapoogopa, mimi ninakutumainia wewe. Ninamutumainia Mungu na kusifu neno lake; ninamutumainia Mungu, wala siogopi. Mwanadamu zaifu atanifanya nini? Muchana kutwa wanatunga maneno juu yangu; mawazo yao yote ni ya kunizuru. Wanakutana kwa kufanya mipango na kunivizia; wanachunguza yote ninayofanya; wanafikiri kwa shabaha ya kunizuru. Ee Mungu, uwalipe kwa kadiri ya uovu wao, uwaangushe hao waovu kwa hasira yako. Wewe unajua kutangatanga kwangu; unaweka machozi yangu ndani ya chupa. Yote yanakuwa katika kitabu chako. Kila mara ninapokuomba musaada wako, waadui zangu wanarudishwa nyuma. Ninajua kweli Mungu yuko upande wangu. Ninamutumainia Mungu na kusifu neno lake; ninamutumainia Yawe na kusifu neno lake. Ninamutumainia Mungu, wala siogopi. Mutu atanifanya nini? Ee Mungu, nitatimiza ahadi zangu kwako; nitakutolea sadaka za shukrani, maana umeniokoa katika kifo, umenilinda nisianguke chini, nipate kuishi mbele yako, ee Mungu, katika mwangaza wa uzima. Kwa mukubwa wa waimbaji. Kwa mutindo wa wimbo “Usiharibu.” Mashairi ya Daudi alipomuponyoka Saulo na kujificha katika pango. Unihurumie, ee Mungu, unihurumie, maana ninakukimbilia wewe. Ninakimbilia kwenye kivuli cha mabawa yako, mpaka zoruba ya maangamizi ipite. Ninamulilia Mungu Mukubwa, Mungu anayenikamilishia nia yake. Atanipelekea musaada toka mbinguni na kuniokoa, atawafezehesha hao wanaonishambulia. Mungu atanionyesha wema na uaminifu wake! Mimi nimezungukwa na waadui, wenye uchu wa damu kama simba; meno yao ni kama mikuki na mishale, ndimi zao ni kama panga kali. Utukuzwe, ee Mungu, juu katika mbingu! Utukufu wako uenee katika dunia yote! Waadui wamenitegea wavu waninase, nami ninaugua kwa huzuni. Wamenichimbia shimo katika njia yangu, lakini wao wenyewe wametumbukia humo. Moyo wangu ni tayari, ee Mungu, moyo wangu ni tayari; nitaimba na kukushangilia! Amuka, ee nafsi yangu! Muamuke, enyi kinubi na zeze! Nitayaamusha mapambazuko! Ee Bwana, nitakushukuru kati ya watu; nitakuimbia sifa kati ya mataifa. Wema wako unaenea hata juu katika mbingu, uaminifu wako unafika hata katika mawingu. Utukuzwe, ee Mungu, juu katika mbingu! Utukufu wako uenee katika dunia yote! Kwa mukubwa wa waimbaji. Kwa mutindo wa wimbo “Usiharibu.” Mashairi ya Daudi. Enyi watawala, munasema kwa haki kweli? Munawahukumu watu kwa usawa? Hapana. Ninyi munafikiria tu kutenda maovu; ninyi wenyewe munaeneza mateso makali katika inchi. Waovu wamepotoka tangu kuzaliwa kwao, hao waongo wamekosa tangu walipozaliwa. Wana sumu kama sumu ya nyoka. Wao ni viziwi kama piri anayeziba masikio, ambaye hasikii hata sauti ya mulozi, au ya muganga anayekuwa fundi wa uchawi. Ee Mungu, uvunje meno yao, uongoe, ee Yawe, meno ya simba wakali hao. Watoweke kama maji yanavyopotelea ndani ya muchanga, kama majani wakanyagwe na kunyauka, watoweke kama konokono anavyoyeyuka akitembea, kama mimba iliyoharibika isiyoona jua hata kidogo! Mbele hawajatambua, waongolewe kama miiba, michongoma au magugu. Kwa hasira ya Mungu, wapeperushwe mbali, wakikuwa bado wazima. Watu wa haki watafurahi wanapoona waovu wanaazibiwa; watatembea katika damu ya watu wabaya. Watu wote watasema: “Kweli, watu wa haki wanapata zawadi! Hakika, kuna Mungu anayehukumu dunia!” Kiebrania: Kwa mukubwa wa waimbaji: kwa mutindo wa wimbo “Usiharibu”. Mashairi ya Daudi wakati Saulo alipotuma wapelelezi wamwue. Ee Mungu wangu, uniokoe kutoka waadui zangu, unikinge na hao wanaonishambulia. Uniokoe na hao wanaotenda maovu, Uniponyeshe kutoka hao wauaji! Angalia! Wananivizia waniue. Watu wakali wanachochea ugomvi juu yangu ingawa sikufanya ubaya wowote. Ingawa sina kosa, wanakimbia, ee Yawe, kujiweka tayari. Uinuke, ee Yawe, uwaangalie na kunisaidia! Uinuke, ee Yawe, Mungu wa majeshi, Mungu wa Israeli. Uamuke, uwaazibu hao watu wasiokujua; usiwaache hao waasi na wabaya. Kila magaribi waadui hao wanarudi wakifoka kama imbwa, na kuzungukazunguka katika muji. Angalia, ni matusi tu yanayotoka katika midomo yao, maneno yao ni kama panga kali; tena wanafikiri hakuna anayewasikia. Lakini wewe, ee Yawe, unawachekelea; unawazarau hao watu wasiokujua. Nitakungojea, ewe unayekuwa nguvu yangu; maana wewe, ee Mungu, ni kimbilio langu. Mungu wangu mwema sana atakuwa mbele yangu, ataniwezesha kuwaona waadui zangu wameshindwa. Usiwaue mara moja, watu wangu wasisahau; uwasambazesambaze kwa nguvu yako, uwaporomoshe chini. Ee Bwana, wewe ndiwe ngao yetu! Wao wanatenda zambi katika masemi yao yote, kwa hiyo wanaswe katika kiburi chao! Kwa sababu ya laana na uongo wao, uwateketeze kwa hasira yako, uwateketeze watoweke kabisa, kusudi watu wote wajue mpaka kwa miisho ya dunia ya kuwa wewe Mungu unatawala wazao wa Yakobo. Kila magaribi waadui hao wanarudi wakifoka kama imbwa, na kuzungukazunguka katika muji. Wanapitapita huko na huko wakitafuta chakula, nao wasiposhiba wananguruma. Lakini mimi nitaimba sifa za nguvu yako, nitashangilia asubui juu ya wema wako, maana wewe umekuwa kikingio changu, wewe ni kimbilio langu wakati wa taabu. Ewe unayekuwa nguvu yangu, nitakuimbia sifa; ee Mungu, wewe ni kikingio changu, Mungu anayenitendea mema! Ee Mungu, umetutupilia na kutuponda, umewaka hasira. Tafazali uturudishie nguvu. Umeitetemesha inchi na kuipasua; uzibe nyufa zake kwa maana imetikisika. Umewaletea watu wako mateso; umetukunywesha divai tuyumbeyumbe. Uwaarifu kwa vitambulisho wale wanaokuheshimu, wapate kuuepuka mushale. Uwaponyeshe hao watu unaowapenda! Utuokoe kwa mukono wako! Utusikilize! Mungu amesema kutoka pahali pake patakatifu: “Sasa kwa shangwe nitaigawanya inchi ya Sekemu; Bonde la Sukoti nitalipima sehemu sehemu. Gileadi ni yangu, na Manase ni yangu; Efuraimu ni kofia yangu ya chuma, na Yuda ni fimbo yangu ya kifalme. Moabu ni kama bakuli langu la kunawia. Nitatupia Edomu kiatu changu kwa kuirizi. Nitapiga kelele la ushindi juu ya Filistia.” Ni nani atakayenipeleka kwenye muji unaozungukwa na kuta? Ni nani atakayeniongoza mpaka Edomu? Si wewe Mungu ambaye umetutupilia? Lakini hauendi tena na jeshi letu. Utusaidie kwa kuwashinda waadui zetu, maana musaada wa mwanadamu haufai kitu. Mungu akikuwa upande wetu, tutashinda. Yeye atawaponda waadui zetu. Kwa mukubwa wa waimbaji. Kwa vyombo vyenye nyuzi. Zaburi ya Daudi. Usikie kilio changu, ee Mungu, usikilize maombi yangu. Ninakulilia kutoka miisho ya dunia, nikikuwa nimevunjika moyo. Uniongoze juu kwenye mulima ambako siwezi kujifikisha. Wewe ndiwe kimbilio langu, boma langu lenye nguvu la kukimbilia waadui. Ninaomba nikae katika nyumba yako milele, nipate kukimbilia chini ya mabawa yako. Ee Mungu, umesikia viapo vyangu, umenijalia sehemu yangu unayowapa wale wanaokuabudu. Umujalie mufalme maisha marefu, miaka yake ikuwe ya vizazi vingi. Atawale milele mbele yako, ee Mungu; wema na uaminifu wako vimulinde. Hivyo nitakuimbia nyimbo za sifa, nikitimiza viapo vyangu kila siku. Kwa mukubwa wa waimbaji. Kwa mutindo wa Yedutuni. Zaburi ya Daudi. Kwa Mungu peke yake ninapata utulivu, wokovu wangu unatoka kwake. Yeye peke yake ndiye kikingio na wokovu wangu, yeye ni kimbilio langu, sitatikisika. Mpaka wakati gani mutanishambulia mimi? Mpaka wakati gani ninyi wote mutanipiga, mimi ninayekuwa kama kiambaza kilichoinama, kama ukuta unaoanza kubomoka? Mumepanga kuniangusha toka nafasi yangu ya heshima; furaha yenu ni kusema uongo. Kwa maneno, munabariki, lakini ndani ya moyo munalaani. Kwa Mungu peke yake ninapata utulivu; tumaini langu linatoka kwake. Yeye peke yake ndiye kikingio na wokovu wangu, yeye ni kimbilio langu, sitatikisika. Wokovu na utukufu wangu vinatoka kwa Mungu; kikingio changu chenye nguvu na kimbilio langu ni Mungu. Enyi watu, mutumainie Mungu siku zote; mumufungulie yanayokuwa ndani ya moyo wenu. Yeye ndiye kimbilio letu. Wanadamu wote ni kama pumzi tu; wote, wakubwa kwa wadogo, hawafai kitu. Wakipimwa wote pamoja, pumzi ni nzito kuliko wao. Musitegemee kutesa, musijisifie mali ya wizi; kama mali zikiongezeka, musizitegemee. Mungu amesema mara na mara, nami nimesikia tena na tena kwamba uwezo ni wa Mungu. Nao wema ni wa Bwana wetu; anamulipa kila mutu kadiri ya matendo yake. Zaburi ya Daudi wakati alipokuwa katika jangwa la Yudea. Ee Mungu, wewe ni Mungu wangu. Moyo wangu unakutafuta, roho yangu inasikia kiu yako, ninasikia kiu yako kama inchi inayokauka kwa ukosefu wa maji. Nina hamu ya kukuona katika pahali pako patakatifu, nione nguvu yako na utukufu wako. Wema wako ni bora kuliko maisha. Nitakusifu kwa midomo yangu. Nitakushukuru maisha yangu yote, nitakuomba nikikuinulia mikono yangu. Roho yangu itafurahi kama mwenye kushiba minofu yenye mafuta, kwa shangwe nitaimba sifa zako. Ninakukumbuka ninapokuwa katika kitanda, ninafikiri juu yako usiku kucha, maana wewe umenisaidia siku zote. Nitashangilia chini ya kivuli cha mabawa yako. Roho yangu inashikamana nawe kabisa; unanilinda kwa mukono wako wa kuume. Lakini hao wanaokusudia kupoteza maisha yangu, watatumbukia chini kwenye makao ya wafu. Watauawa kwa upanga, maiti zao zikuwe chakula cha mbweha. Lakini mufalme atamufurahia Mungu; nao wote wanaoapa kwa jina la Mungu watamusifu, lakini vinywa vya waongo vitafungwa. Kwa mukubwa wa waimbaji. Zaburi ya Daudi. Wimbo. Ee Mungu, usikilize malalamiko yangu. Uyalinde maisha yangu kutoka vitisho vya waadui. Unikinge na shauri baya la waovu, nayo fujo ya watu wabaya. Wananoa ndimi zao kama upanga, nayo maneno yao ni makali kama mishale. Wanapiga mutu mukamilifu kwa uficho, wanamupiga kwa rafla bila kuogopa. Wanashirikiana katika nia yao mbaya; wanapatana pahali pa kuficha mitego yao. Wanajisemesha: “Hakuna atakayeweza kuiona.” Wanafanya shauri baya wakijisemesha: “Tumetimiza sasa mipango yetu! Nani anayeweza kugundua mafikiri ya ndani ya mutu?” Lakini Mungu atawapiga mishale, na kuwaumiza kwa rafla. Atawaangamiza kwa sababu ya maneno yao; kila atakayewaona atatikisa kichwa. Hapo watu wote wataogopa; watatangaza kazi Mungu aliyoifanya, na kufikiri juu ya matendo yake. Watu wa haki watamufurahia Yawe, na kukimbilia kwake; watu wote wenye moyo wa usawa watamusifu. Kwa mukubwa wa waimbaji. Zaburi. Wimbo wa Daudi. Ee Mungu, unastahili sifa huko Sayuni. Watu wanapaswa kukutimizia viapo vyao, maana wewe unajibu maombi yetu. Wanadamu wote watakuja kwako wewe peke. Tunapolemewa na makosa yetu, wewe mwenyewe unatusamehe. Heri wale unaowachagua na kuwaleta karibu, waishi katika kiwanja chako. Sisi tutatoshelewa na mazuri ya nyumba yako, mazuri ya hekalu lako takatifu. Kwa matendo yako makubwa unatuitikia na kutuokoa, ewe Mungu mwokozi wetu. Wewe ndiwe tumaini la viumbe vyote katika dunia yote na mbali katika bahari. Kwa nguvu yako uliisimika milima pahali pake. Wewe una nguvu nyingi! Unatuliza uvumi wa bahari na wa mawimbi yake, unakomesha fujo za watu. Wakaaji wa miisho ya dunia wanashangazwa na vitambulisho vyako. Unasababisha furaha kila pahali, tokea mashariki hata magaribi. Wewe unatunza udongo kwa kuunyeshea mvua, unaujalia mboleo na kuustawisha; muto wako umejaa maji tele, unaifanikisha inchi na kuipatia mavuno. Hivi ndivyo unavyotayarisha udongo. Unanyeshea mashamba mvua kwa wingi, na kuyalowanisha kwa maji; unalainisha udongo kwa manyunyu, na kubariki mimea ichipuke. Unakamilisha mwaka kwa kutupatia mazao mazuri; kila nafasi ulipopita kumejaa utajiri. Mbuga za majani zimejaa mifugo, milima nayo imejaa furaha. Mashamba ya kulishia nyama yamejaa kondoo, mabonde yamefunikwa na ngano. Kila kitu kinashangilia kwa furaha. Kwa mukubwa wa waimbaji. Wimbo. Zaburi. Enyi wakaaji wote wa dunia, mumushangilie Mungu! Muimbe kwa ajili ya utukufu wa jina lake, mumusifu kwa utukufu! Mumwambie Mungu: “Matendo yako ni ya ajabu! Kwa nguvu yako kubwa waadui zako wanaishiwa nguvu. Dunia yote inakuabudu; watu wote wanakuimbia sifa!” Mukuje muone mambo Mungu aliyotenda; ametenda mambo ya kutisha kati ya watu. Aligeuza bahari kuwa inchi kavu, watu wakapita humo kwa miguu; kwa hiyo nasi tukashangilia. Anatawala milele kwa nguvu yake kubwa; macho yake yanachungulia mataifa yote. Mwasi yeyote asisubutu kumupinga. Mumusifu Mungu wetu, enyi mataifa yote; mutangaze sifa zake zipate kusikilika. Yeye ametujalia maisha, wala hakutuacha tuanguke. Umetupima, ee Mungu, umetujaribu kama madini kwa moto. Umetunasa katika wavu; umetubebesha muzigo muzito. Umewaacha watu watukanyage; tumepitia katika moto na katika maji. Lakini sasa umetuleta kwenye usalama. Nitakuja ndani ya nyumba yako na sadaka za kuteketezwa, nitakutimizia viapo vyangu nilivyotamka na kukuahidia mimi mwenyewe nilipokuwa katika taabu. Nitakutolea sadaka za kuteketezwa za nyama wenye kunona, sadaka za kuteketezwa za kondoo dume; nitatoa sadaka za ngombe dume na beberu. Enyi munaomwabudu Mungu, mukuje wote musikilize, nami nitawaelezea mambo aliyonitendea. Mimi nilimulilia kwa sauti, sifa zake nikazitangaza. Kama ningalikusudia maovu ndani ya moyo, Yawe hangalinisikiliza. Lakini kweli Mungu amenisikiliza; amesikiliza maneno ya maombi yangu. Mungu asifiwe! Hakukataa maombi yangu, wala hakuacha kunitendea mema. Kwa mukubwa wa waimbaji. Kwa vyombo vyenye nyuzi. Zaburi. Wimbo. Utuonee huruma, ee Mungu, utubariki, utuelekezee uso wako kwa wema, dunia yote ipate kutambua njia yako, mataifa yote yajue nguvu yako ya kuokoa. Watu wakusifu, ee Mungu, watu wote wakusifu! Mataifa yote yafurahi na kuimba kwa furaha; maana unawahukumu watu kwa usawa, na kuyaongoza mataifa katika dunia. Watu wakusifu, ee Mungu, watu wote wakusifu! Inchi imetoa mazao yake; Mungu, Mungu wetu, ametubariki. Mungu aendelee kutubariki. Watu wote katika dunia wamwabudu. Kwa mukubwa wa waimbaji. Zaburi ya Daudi. Mungu asimame sasa, na waadui zake watawanyike! Wanaomuchukia wakimbie mbali naye! Kama moshi unavyopeperushwa na upepo, ndivyo nao wanavyopeperushwa; kama inta inavyoyeyuka karibu na moto, ndivyo waovu wanavyoangamia mbele ya Mungu! Lakini watu wa haki wanafurahi Mungu anapokuja, wanashangilia na kuimba kwa furaha. Mumwimbie Mungu, musifu jina lake; mumutengenezee njia yeye anayetembea juu ya mawingu. Jina lake ni Yawe; mufurahi mbele yake. Mungu anayekaa pahali pake patakatifu, ni Baba ya wayatima na mulinzi wa wajane. Mungu anawapatia wenye ukiwa jamaa, anawafungua wafungwa na kuwapa uheri. Lakini waasi wataishi katika inchi yenye kukauka. Ee Mungu, ulipowaongoza watu wako, uliposafiri kule katika jangwa, dunia ilitetemeka, mbingu zilitiririsha mvua; mbele yako, Mungu wa Sinai, mbele yako, Mungu wa Israeli! Ee Mungu, ulinyeshea inchi mvua nyingi, ulitia tena inchi yako nguvu ilipokuwa imechakaa. Watu wako wakapata makao ndani yake, uliyotayarishia wamasikini kwa uzuri wako. Bwana alitoa amri, nao wanawake wengi wakatangaza habari: “Wafalme na majeshi yao wanakimbia ovyo!” Wanawake waliobaki ndani ya nyumba waligawanya vitu vilivyonyanganywa, ingawa walibaki ndani ya mazizi: sanamu za njiwa zilizotengenezwa na feza, na mabawa yao yanayoangaa zahabu. Mungu Mukubwa alipowatawanya wafalme, teluji ilianguka juu ya mulima Salmoni. Ewe mulima wa Basani, murefu na wenye vichwa vingi, mbona unauonea kijicho mulima Mungu aliouchagua akae juu yake? Yawe atakaa huko milele! Bwana anakuja kwenye pahali pake patakatifu kutoka Sinai, akikuwa na kundi kubwa, na maelfu na maelfu ya magari ya kukokotwa. Anapanda juu akichukua wafungwa, anapokea zawadi kutoka kwa watu, hata kutoka kwa watu walioasi, Yawe apate kukaa huko. Yawe asifiwe siku kwa siku! Yeye anatubebea mizigo yetu, yeye ndiye Mungu mwokozi wetu. Mungu wetu ni Mungu mwenye kutuokoa; Bwana wetu Yawe pekee ndiye anayeokoa katika kifo. Mungu ataviponda vichwa vya waadui zake, ndivyo vichwa vya wanaoendelea katika njia mbaya. Bwana wetu alisema: “Nitawarudisha waadui kutoka Basani; nitawarudisha kutoka shimo la bahari, usafishe miguu katika damu ya waadui zako, nao imbwa wako wapate posho yao.” Ee Mungu, maandamano yako ya ushindi yanaonekana; maandamano ya Mungu wangu, mufalme wangu, katika pahali patakatifu! Mbele waimbaji, nyuma wanamuziki, katikati wabinti wanavumisha ngoma. “Mumusifu Mungu katika mukutano. Mumusifu Yawe, enyi wazao wa Israeli!” Kwanza ni Benjamina, mudogo wa wote; kisha waongozi wa Yuda na kundi lao, halafu wakubwa wa Zebuluni na Nafutali. Onyesha, ee Mungu, nguvu yako kubwa; nguvu yako uliyotumia kwa ajili yetu. Kutoka katika hekalu lako, Yerusalema, ambapo wafalme watakufikia na zawadi zao, uwakaripie wale nyama wanaokaa katika matete, kundi la mabeberu na ngombe dume, mpaka mataifa hayo yakupe heshima na kodi. Uwatawanye hao watu wenye kupenda vita! Wajumbe watakuja kutoka Misri, Waetiopia watamuletea Mungu mali zao. Enyi falme za dunia, mumwimbie Mungu, mumwimbie Bwana wetu nyimbo za sifa, mumwimbie yeye anayepita katika mbingu, mbingu za tangu zamani. Mumusikilize akinguruma kwa kishindo. Mutambue nguvu za Mungu; yeye anatawala juu ya Israeli, mamlaka yake yanafika katika mbingu. Mungu ni wa kutisha tangia pahali pake patakatifu, yeye ni Mungu wa Israeli! Anawapa watu wake nguvu na uwezo. Mungu asifiwe! Kwa mukubwa wa waimbaji. Kwa mutindo wa wimbo “Mayungiyungi.” Zaburi ya Daudi. Uniokoe, ee Mungu; maji yamenifikia katika shingo. Ninazama ndani ya matope mengi, hakuna pahali pa kuweka miguu. Nimetumbukia kwenye shimo refu la maji, ninachukuliwa na maji mengi. Ninaregea kwa ajili ya kulalamika, na koo langu limekauka. Macho yangu yamefifia, nikikungojea ewe Mungu wangu. Watu wengi kuliko nywele zangu wananichukia. Wana nguvu sana hao wanaotaka kuniua, hao wanaonishambulia kwa mambo ya uongo. Nirudishe kitu ambacho sikuiba? Ee Mungu, unajua upumbafu wangu; makosa yangu hayafichwi mbele yako. Wanaokutumainia wasifezeheke kwa sababu yangu, ee Bwana wetu, Yawe wa majeshi; wanaokutafuta, wasizarauliwe kwa sababu yangu, ee Mungu wa Israeli. Kwa ajili yako ninavumilia matusi; haya imefunika uso wangu. Nimekuwa mugeni kwa wandugu zangu, kaka na dada zangu hawanitambui. Upendo wangu kwa ajili ya nyumba yako unanichoma. Matusi wanayokutukana yananiangukia. Nilipojinyenyekeza kwa kufunga kula chakula, watu walinilaumu. Nilipovaa gunia kwa kuomboleza, nikageuka kuwa wimbo kwao. Nimekuwa kichekesho kwa watu katika barabara; walevi wanatunga nyimbo juu yangu. Lakini mimi ninakuomba wewe, ee Yawe. Ee Mungu, ukubali maombi yangu wakati unaopenda. Kwa wingi wa wema wako unijibu. Wewe mukombozi anayestahili kuaminiwa, uniokoe nisizame katika matope; uniokoe na hao wanaonichukia, unilinde salama kutoka shimo refu la maji. Usiniache nipelekwe na maji mengi, au nizame kwenye shimo lake, au nimezwe na kifo. Ee Yawe, unijibu, unielekee, kwa uzuri wa wema wako, kwa wingi wa rehema yako. Usimugeuzie mutumishi wako mugongo, unijibu haraka, maana niko katika hatari. Unisogelee karibu na kunikomboa, uniokoe na waadui zangu wengi. Wewe unajua ninavyotukanwa, unajua haya na matusi ninazopata; na waadui zangu wote wewe unawajua. Matusi yamevunja moyo wangu, nami nimekata tamaa. Nimetafuta kitulizo lakini sikupata, nimetafuta wa kunifariji lakini sikumupata. Walinipa sumu ndani ya chakula, na nilipokuwa na kiu wakanipa divai inayochacha. Karamu zao zikuwe mutego kwao, na sikukuu zao ziwanase. Macho yao yatiwe giza wasiweze kuona, uikunje siku zote migongo yao. Uwamwangie hasira yako, kasirani yako iwaangukie. Kambi zao ziachwe matongo, mutu yeyote asiishi katika mahema yao. Maana wanamutesa yule uliomwazibu, wanawaongezea maumivu wale uliowaumiza. Uwaazibu kwa kila uovu wao; ukatae kabisa kuwasamehe. Uwafute katika kitabu cha wenye kuishi, wasikuwe katika hesabu ya watu wa haki. Lakini mimi ninayekuwa muzaifu na mugonjwa, uniinue juu, ee Mungu, uniokoe. Kwa wimbo nitalisifu jina la Mungu, nitamutukuza kwa shukrani. Jambo hili litamupendeza Yawe zaidi, kuliko kumutolea sadaka ya ngombe, kuliko kumutolea ngombe dume muzima. Wanyenyekevu wataona hayo na kufurahi; wanaomutafuta Mungu watapata moyo. Yawe anawasikiliza wakosefu; hatawasahau hata kidogo watu wake wafungwa. Enyi mbingu na dunia, mumusifu Mungu; bahari na vyote vinavyokuwa ndani yenu, mumusifu. Maana Mungu ataokoa Sayuni, na kuijenga tena miji ya Yuda. Watu wake wataishi humo na kuirizi; wazao wa watumishi wake watairizi, wale wanaopenda jina lake wataishi humo. Kwa mukubwa wa waimbaji. Zaburi ya Daudi inayoelekea sadaka yake ya ukumbusho. Ee Mungu, uniokoe! Ee Yawe, ukuje haraka unisaidie. Wapate haya na kufezeheka wanaotaka kuniua! Warudi nyuma na kufezeheka wanaonitakia hasara! Wapumbazike kwa haya, hao wanaofurahia kunizomea! Lakini wote wanaokutafuta, wafurahi na kushangilia kwa sababu yako. Wote wanaopenda wokovu wako, waseme siku zote: “Mungu ni mukubwa!” Nami ninayekuwa masikini na mukosefu, unifikie haraka, ee Mungu! Wewe ndiwe musaada wangu na mukombozi wangu. Ee Yawe, usikawie! Ninakimbilia kwako, ee Yawe, usiniachilie kufezeheka hata kidogo! Kwa haki yako uniokoe na kunikomboa; unitegee sikio lako na kuniokoa! Ukuwe kikingio changu cha kukimbilia, kimbilio lenye nguvu la kuniokoa, kwa maana wewe ni kikingio na kimbilio langu. Uniokoe, ee Mungu wangu, kutoka mikono ya waovu, kutoka makucha ya watu wabaya na wakali. Maana wewe, Bwana wangu Yawe, ni tumaini langu, tegemeo langu tangu ujana wangu. Nimekutegemea tangu kuzaliwa kwangu; wewe ulinilinda nilipotoka katika tumbo la mama yangu. Nitakusifu siku zote. Kwa wengi nimekuwa mushangao, lakini wewe ni kimbilio langu lenye nguvu. Kinywa changu kimejaa sifa zako, na utukufu wako muchana kutwa. Wakati wa uzee usinitupe; ninapoishiwa na nguvu usiniachilie. Maana waadui zangu wanasema vibaya juu yangu; wanaovizia maisha yangu wanafanya mipango, na kusema: “Mungu amemwachilia; mumufuate na kumukamata, kwa maana hakuna wa kumwokoa!” Usikae mbali nami, ee Mungu; ukuje haraka unisaidie, ee Mungu wangu. Wapinzani wangu wote wafezeheke na kuangamizwa; wenye kuvizia kuniua wafezeheke na kuzarauliwa. Lakini mimi nitakuwa na matumaini siku zote; tena nitakusifu zaidi na zaidi. Kinywa changu kitaeleza matendo yako ya haki, nitatangaza muchana kutwa matendo yako ya wokovu ijapokuwa hayo yanapita akili yangu. Nitataja matendo yako makubwa, ee Bwana wangu Yawe; nitatangaza kwamba wewe ndiwe mwenye haki. Ee Mungu, wewe umenifundisha tangu ujana wangu; tena na tena, ninatangaza matendo yako ya ajabu. Usiniachilie, ee Mungu, nitakapokuwa muzee mwenye imvi nyingi, kusudi nivitangazie vizazi vitakavyokuja nguvu yako. Nguvu na haki yako, ee Mungu, vinafika mpaka juu katika mbingu. Wewe umefanya mambo makubwa sana. Ee Mungu, ni nani anayekuwa kama wewe? Umeniletea taabu kubwa, lakini utanirudishia tena uzima, wewe utaniinua tena kutoka katika shimo. Utaniongezea heshima yangu, na kunifariji tena. Nami nitakusifu kwa kinubi, kwa sababu ya uaminifu wako, ee Mungu wangu; nitakuimbia sifa kwa zeze, ewe Mutakatifu wa Israeli. Nitanyanyua sauti kwa furaha, ninapokuimbia wewe sifa zako, na roho yangu itakusifu, maana umeniokoa. Nitatangaza haki yako muchana kutwa, maana wanaonitakia hasara wamefezeheka na kuzarauliwa. Zaburi ya Solomono. Ee Mungu, umujalie mufalme uwezo wa kufuata sheria yako, umupe mwana wa mufalme haki yako. Atawale taifa lako kwa haki, na wamasikini wako kwa sheria yako. Milima ilete ustawi kwa watu wako, vilima vijae haki. Mufalme awatetee wamasikini wa taifa, awasaidie wakosefu, na kuwaangamiza watesaji. Mufalme aishi muda murefu kama jua, na kama mwezi, kwa vizazi vyote. Akuwe kama manyunyu yanayolowanisha mashamba, kama mvua inayonyeshea udongo. Haki istawi maisha yake yote, na amani kwa wingi mpaka mwezi ukome. Atawale kutoka bahari hata bahari, kutoka muto Furati hata miisho ya dunia. Waadui zake wanaokaa katika jangwa wanyenyekee mbele yake, wapinzani wake walambule vumbi. Wafalme wa Tarsisi na visiwa wamulipe kodi, wafalme wa Sheba na Seba wamuletee zawadi. Wafalme wote wa dunia wamuheshimu, watu wa mataifa yote wamutumikie. Atamukomboa mukosefu anayemwomba, na masikini asiyekuwa na wa kumusaidia. Atawahurumia wazaifu na wakosefu, atayaokoa maisha yao wenye shida. Atawatoa katika mateso na ukali, maana maisha yao ni ya bei kubwa kwake. Mufalme aishi maisha marefu; apokee zawadi ya zahabu kutoka Sheba; watu wamwombee kwa Mungu siku zote, na kumutakia baraka muchana kutwa. Inchi itoe mazao kwa wingi, vilima vijae mavuno kama ya Lebanoni, na watu wa miji wastawi kama majani. Jina la mufalme litukuzwe siku zote; utukufu wake udumu muda wote jua litakapokuwa. Kwake mataifa yote yabarikiwe; watu wote wamwite mwenye heri! Atukuzwe Yawe, Mungu wa Israeli, ambaye peke yake anafanya miujiza. Jina lake tukufu litukuzwe milele; utukufu wake ujae katika ulimwengu wote! Amina, Amina! Mwisho wa maombi ya Daudi mwana wa Yese. Zaburi ya Asafu. Hakika, Mungu ni muzuri kwa Israeli, kwa watu wenye moyo safi. Nilikuwa karibu sana kujikwaa, kidogo tu ningeteleza, maana niliwaonea wivu wenye kiburi, nilipoona wakosaji wakifanikiwa. Maana hao hawapatwi na mateso; miili yao ina afya, nao wana nguvu. Taabu za mwanadamu haziwapati hao; hawapati mateso kama watu wengine. Kiburi kimekuwa kama mukufu katika shingo, mateso makali ni kama nguo yao. Mazarau yanatokana na unene wao; mioyo yao inatiririka mipango mibaya. Wanawachekelea wengine na kusema mabaya; wanajivuna na kufanya mipango ya utesaji. Kwa vinywa vyao wanatukana mbingu; kwa ndimi zao wanajitapa katika dunia. Hata watu wa Mungu wanawafuata, hawaoni kwao kitu chochote kibaya na kusadiki kila wanachosema. Wanasema: “Mungu hawezi kujua! Mungu Mukubwa hataweza kugundua!” Hivi ndivyo watu waovu wanavyokuwa; wako na kila kitu, nao wanapata hata zaidi. Kweli ni kwa bure nimejichunga katika usafi wa moyo, na kujilinda nisitende zambi? Muchana kutwa ninapata mapigo, kila asubui nimepata mateso. Ningalisema kama wao, ningalikuwa mwenye uasi kati ya watu wako. Basi, nilijaribu kufikiri juu ya jambo hili, lakini lilikuwa gumu sana kwangu, mpaka nilipoingia pahali pako patakatifu. Halafu nikatambua yatakayowapata waovu. Kweli wewe unawaweka pahali penye utelezi; unawafanya waanguke na kuangamia. Wanaangamizwa kwa rafla, wateketezwe kabisa kwa vitisho. Ee Bwana, unapoinuka, wanatoweka kama ndoto, kama ndoto wakati mutu anapoamuka. Nilipoona uchungu katika moyo na kuchomwa katika roho, nilikuwa mupumbafu na mujinga, nilikuwa kama nyama mbele yako. Hata hivyo siku zote niko nawe, ee Mungu! Unanishika mukono wa kuume. Wewe unaniongoza kwa mashauri yako; na kwa mwisho utanipokea kwenye utukufu. Mbinguni, nani anayeweza kunisaidia isipokuwa wewe? Na katika dunia hamuna ninachokitamani isipokuwa wewe! Hata nikikosa nguvu katika mwili na katika roho, wewe, ee Mungu, ni kikingio changu; na hitaji langu lote ni wewe kwa milele. Anayejitenga nawe, hakika ataangamia. Anayekukana, utamwangamiza. Lakini, kwangu ni vizuri kuwa karibu na Mungu. Wewe Bwana wangu Yawe ndiwe usalama wangu. Nitatangaza mambo yote uliyotenda! Mashairi ya Asafu. Kwa nini, ee Mungu, umetutupilia kabisa? Mbona hasira yako inawaka juu ya kondoo wako? Kumbuka taifa lako ulilojipatia tangia zamani, kabila ulilokomboa likuwe mali yako. Kumbuka mulima Sayuni pahali unapokaa. Pita juu ya mabomoko haya ya tangu zamani! Waadui wameharibu kila kitu katika hekalu. Waadui zako wamepiga kelele la ushindi katika hekalu lako! Wamesimika humo bendera zao za ushindi! Wanafanana na mukataji wa kuni, anayekata miti kwa shoka lake. Walivunjavunja michoro ya hekalu, kwa mashoka na nyundo zao. Waliunguza pahali patakatifu pako; walikufuru pahali pale unapoheshimiwa. Walikusudia kutuangamiza wote pamoja; walichoma pahali pote katika inchi ambapo tulikutana kwa kukuabudu. Hatuoni tena vitambulisho vya kuwa kwako kati yetu, hatuna tena nabii yeyote, wala hakuna anayejua mwisho wa haya yote! Ee Mungu, mpaka wakati gani adui atakuchekelea? Watakufuru jina lako milele? Mbona umeficha mukono wako wa kuume? Kwa nini haunyooshi mukono na kuwapiga? Hata hivyo wewe Mungu ni mufalme wetu tangu zamani; umefanya mambo makubwa ya kuokoa katika inchi. Kwa uwezo wako mukubwa uligawanya bahari; uliponda vichwa vya nyama mukubwa wa bahari. Wewe uliponda vichwa vya nyama mukubwa Leviatani; ukawapa wanyama wa jangwa muzoga wake. Wewe umefanya chemichemi na vijito; na kukausha mito mikubwa. Muchana ni wako na usiku ni wako; umeweka mwezi na jua kwenye nafasi zao. Wewe umeweka mipaka yote ya dunia; umepanga wakati wa kipwa na wakati wa mvua. Kumbuka, ee Yawe, mazarau ya waadui zako; taifa pumbafu linatukana jina lako. Usitutupie, sisi njiwa wako, kwa wanyama wakali, usisahau kwa siku zote maisha ya wamasikini wako. Ukumbuke agano ulilofanya nasi! Inchi imejaa mateso makali kila nafasi za giza. Usiwaache wanaogandamizwa wafezeheshwe, uwajalie wamasikini na wakosefu wasifu jina lako. Ee Mungu, simama sasa ujitetee! Ukumbuke mazarau ya kila siku ya wasiokujua. Usisahau makelele ya waadui zako; na fujo ya siku zote ya wapinzani wako. Kwa mukubwa wa waimbaji: kwa mutindo wa wimbo “Usiharibu”. Zaburi ya Asafu: wimbo. Tunakushukuru, ee Mungu, tunakushukuru! Tunatangaza ukubwa wa jina lako na kueleza matendo yako makubwa. Mungu anasema: “Mimi nimeweka wakati kamili! Wakati huo nitahukumu kwa haki. Inchi ikitetemeka na vyote vinavyokuwa ndani yake, mimi ndiye ninayeimarisha misingi yake. Ninawaambia wenye kiburi: ‘Mwache kiburi’, na waovu: ‘Musiote mapembe! Musijione kuwa watu wa maana sana, wala kusema maneno ya majivuno.’ ” Ukubwa hautoki mashariki au magaribi, wala hautoki katika jangwa au kwa milima. Mungu mwenyewe ndiye mwamuzi; anamushusha mumoja na kumwinua mwingine. Yawe anashika kikombe katika mukono, kimejaa divai kali ya hasira yake. Anaimimia, nao waovu wote wanaikunywa; wanaikunywa mpaka tone la mwisho. Lakini mimi nitafurahi milele, nitamwimbia Mungu wa Yakobo sifa. Atavunja mapembe yote ya watu waovu; lakini ataotesha mapembe ya watu wa haki. Kwa mukubwa wa waimbaji: kwa vyombo vyenye nyuzi. Zaburi ya Asafu. Wimbo. Mungu anajulikana katika Yuda; jina lake ni kubwa katika Israeli. Makao yake ni kule Salemu; nyumba yake ni kule Sayuni. Kule alivunja mishale ya waadui; alivunja ngao, panga na silaha za vita. Ee Mungu, wewe unatukuzwa sana; unajaa utukufu kuliko milima ya milele. Wenye nguvu wamenyanganywa, sasa wamelala usingizi wa kifo, washujaa wa vita hawakuweza kutumia mikono yao. Ulipowakaripia, ee Mungu wa Yakobo, farasi na wapanda-farasi walipooza. Wewe, ee Mungu, ni wa kutisha sana! Nani anayeweza kusimama mbele yako ukikasirika? Ulijulisha hukumu yako toka mbinguni. Dunia iliogopa na kunyamaza, wakati ulipoinuka kutimiza hukumu, kuwaokoa wote wanaoteswa katika dunia. Kasirani ya watu inasababisha tu sifa yako; walioponyoka katika vita watafanya sikukuu zako. Mumutimizie Yawe, Mungu wenu, ahadi zenu; enyi munaokuwa karibu, mumupe zawadi Mungu wa kutisha. Yeye anavunja kiburi cha wakubwa; anawatisha wafalme wa dunia. Kwa mukubwa wa waimbaji: kwa mutindo wa Yedutuni. Zaburi ya Asafu. Ninamulilia Mungu kwa sauti. Kwa sauti ninamulilia Mungu, anisikie. Wakati wa taabu ninamutafuta Bwana wetu; ninamunyooshea mikono yangu usiku bila kuchoka, lakini sifarijiwi na mutu yeyote. Ninafikiri juu ya Mungu na kuugua; ninamukumbuka na kufa moyo. Unanizuiza hata kupata usingizi, ninahangaika hata siwezi kusema. Ninafikiri juu ya siku za zamani; ninakumbuka miaka ya hapo kale. Usiku ninawazawaza; moyo wangu unafikiri, nayo roho yangu inajiuliza: “Bwana ametuachilia kabisa? Hatapendezwa tena nasi? Wema wake umekwisha kabisa? Hatatimiza tena ahadi zake? Mungu amesahau kuwa na huruma? Hasira yake imeondoa rehema yake?” Kisha nikasema: “Kinachoniumiza zaidi ni kwamba Mungu Mukubwa hatendi tena kitu kwa ajili yetu!” Nitayakumbuka matendo yako, ee Yawe, nitafikiri juu ya maajabu yako ya hapo kale. Ninafikiri juu ya kazi zako, ninawaza juu ya matendo yako makubwa. Kila unachofanya, ee Mungu, ni kitakatifu. Ni mungu gani anayekuwa mukubwa kama Mungu wetu? Wewe ni Mungu unayetenda maajabu; wewe umeyaonyesha mataifa uwezo wako. Kwa mukono wako wa kuume uliwakomboa watu wako; uliwakomboa wazao wa Yakobo na Yosefu. Maji yalipokuona, ee Mungu, maji yalipokuona, yaliogopa sana; bahari ilitetemeka mpaka chini. Mawingu yalinyesha mvua nyingi, ngurumo zikavuma katika anga, mishale ya umeme ikaangaza kila upande. Kishindo cha ngurumo yako kilitokea katika zoruba, umeme wako ukaangaza ulimwengu, dunia ikatikisika na kutetemeka. Wewe ukajifanyia njia juu ya bahari; ulitembea juu ya maji yale mengi, lakini pahali ulipopita hapakuonekana. Uliwaongoza watu wako kama kondoo, chini ya uongozi wa Musa na Haruni. Mashairi ya Asafu. Musikie mafundisho yangu, enyi watu wangu, mutegee sikio maneno ya kinywa changu. Nitasema nanyi kwa mafumbo, nitasema mambo yaliyofichwa tangu zamani; mambo tuliyosikia na kuyajua, mambo ambayo babu zetu walituelezea. Hatutayaficha kwa watoto wetu lakini tutawaelezea kizazi kinachokuja matendo ya utukufu ya Yawe na uwezo wake; tutawaambia maajabu yake aliyotenda. Aliwapa wazao wa Yakobo masharti, aliweka sheria katika Israeli ambayo aliwaamuru babu zetu wawafundishe watoto wao; kusudi watu wa kizazi kinachokuja, watoto watakaozaliwa kisha, wazijue, nao pia wawajulishe watoto wao, kusudi wamwekee Mungu tumaini lao, wasipate kusahau matendo ya Mungu, lakini washike amri zake, wasikuwe kama vile babu zao walivyokuwa, watu wagumu na waasi, kizazi ambacho hakikuwa na musimamo kamili, ambacho hakikuwa na uaminifu kwa Mungu. Watu wa Efuraimu, pinde na mishale katika mukono, walirudi nyuma, wakakimbia siku ile ya vita. Hawakushika agano la Mungu; walikataa kufuata sheria yake. Walisahau mambo aliyokuwa ametenda, ndiyo miujiza aliyokuwa amewaonyesha. Alifanya maajabu mbele ya babu zao, katika mbuga za Soani kule Misri. Aligawanya bahari, akawapitisha ndani yake; aliyafanya maji yasimame kama ukuta. Muchana aliwaongoza kwa wingu; usiku kucha kwa mwangaza wa moto. Alipasua mawe kule katika jangwa, akawakunywesha maji kutoka shimo refu. Alitiririsha vijito kutoka katika jiwe, nayo maji kama mito. Hata hivyo waliendelea kumukosea Mungu; walimwasi Mungu Mukubwa kule katika jangwa. Walimujaribu Mungu kwa makusudi; wakidai wapewe chakula walichotaka. Walimutukana Mungu wakisema: “Hakika, Mungu anaweza kutupatia chakula katika jangwa? Ni kweli, alipiga jiwe, maji yakatiririka kama muto; lakini, sasa anaweza kweli kutupatia mukate, na kuwapatia watu wake nyama?” Yawe, aliposikia hayo, akakasirika, moto ukawawakia wazao wa Yakobo, hasira yake ikapanda juu ya watu wa Israeli, kwa sababu hawakumwaminia, wala hawakutumainia kwamba angeweza kuwaokoa. Hata hivyo aliamuru mawingu, akafungua milango ya mbingu; akawanyeshea mana wapate kula, akawapa ngano kutoka mbinguni. Wanadamu wakakula chakula cha wamalaika; naye aliwapelekea chakula cha kutosha. Alivumisha upepo wa mashariki, kwa nguvu yake akachochea upepo wa kusini, akawaangushia watu wake nyama kama vumbi, ndege wengi kama muchanga wa bahari. Ndege hao walianguka katika kambi lao, kandokando ya makao yao. Watu walikula wakashiba; Mungu aliwapa walichotaka. Lakini mbele ya kukata hamu yao, chakula kilipokuwa kingali katika kinywa, hasira ya Mungu iliwaka juu yao; akaua wenye nguvu kati yao, na kuwaangusha vijana wa Israeli. Hata hivyo waliendelea kumukosea Mungu; ijapokuwa alitenda maajabu, hawakuamini. Basi, akatowesha siku zao kama pumzi, miaka yao kwa misiba ya rafla. Kila mara alipowaua, waliobaki walimugeukia; wakageuka toka ubaya wao, wakamugeukia Mungu kwa moyo. Walikumbuka kwamba Mungu alikuwa kikingio chao, kwamba Mungu Mukubwa alikuwa mukombozi wao. Lakini walimudanganya kwa maneno yao; walimwambia uongo. Hawakuambatana naye kwa moyo, hawakukuwa waaminifu kwa agano lake. Lakini Mungu mwenye huruma alisamehe uovu wao, wala hakuwaangamiza. Mara nyingi alizuia hasira yake, wala hakuacha kasirani yake yote iwake. Alikumbuka kwamba wao ni watu tu; ni kama upepo unaopita na kutoweka. Mara ngapi walimwasi kule katika jangwa, na kumuchukiza huko kwenye ukiwa! Walimujaribu Mungu tena na tena, wakamukasirikisha huyo Mutakatifu wa Israeli. Hawakukumbuka nguvu yake, wala siku ile alipowaokoa kutoka waadui zao, alipotenda maajabu katika inchi ya Misri, na miujiza katika mbuga za Soani! Aligeuza ile mito kuwa damu, Wamisri wasipate maji ya kunywa. Aliwapelekea makundi ya mainzi yaliyowasumbua, na vyura waliowaletea hasara. Alituma nzige, wakakula mavuno yao, na kuharibu mashamba yao. Aliiharibu mizabibu yao kwa mvua ya mawe, na mitini yao kwa baridi kali. Ngombe wao aliwaua kwa mvua ya mawe, na kondoo wao kwa radi. Alimwanga juu yao hasira yake kali, kasirani, chuki na taabu, na kuwashushia kundi la wamalaika waangamizaji. Aliachilia hasira yake iendelee, wala hakuwaepusha na kifo, lakini aliwaangamiza kwa ugonjwa mukali. Aliwaua wazaliwa wa kwanza wote wa Wamisri; ndilo chipukizi la kwanza katika kambi la Hamu. Kisha aliwahamisha watu wake kama kondoo, akawaongoza katika jangwa kama kundi la nyama. Aliwaongoza salama, wala hawakuogopa; lakini bahari iliwafunika waadui zao. Aliwaleta katika inchi yake takatifu, katika mulima aliounyanganya kwa nguvu yake. Alifukuza mataifa mbele yao, akatoa inchi zao zikuwe mali ya Israeli, akaikalisha makabila ya Israeli katika mahema zao. Hata hivyo walimupima na kumwasi Mungu Mukubwa; wala hawakushika maagizo yake. Lakini waligeuka na kufanya mabaya kama babu zao; wakayumbayumba kama upinde usiokuwa imara. Walimukasirikisha kwa mazabahu zao za miungu; wakamutia wivu kwa sanamu zao za kuchongwa. Mungu alipoona hayo, akawaka hasira; akamukataa Israeli kabisa. Aliacha makao yake kule Shilo, makao ambamo alikaa kati ya watu. Aliacha kitambulisho cha nguvu yake kinyanganywe, utukufu wake utiwe katika mikono ya waadui. Aliwakasirikia watu wake mwenyewe; akawatoa waangamizwe kwa upanga. Moto ukawateketeza vijana wao wanaume, na wabinti wao wakakosa wachumba. Makuhani wao walikufa kwa upanga, wala wajane wao hawakuomboleza. Kisha Bwana aliamuka kama kutoka katika usingizi, kama shujaa aliyechangamushwa na divai. Akawashinda waadui zake; akawafezehesha kwa milele. Alikataa wazao wa Yosefu, wala hakuchagua kabila la Efuraimu. Lakini alichagua kabila la Yuda, mulima Sayuni anaoupenda. Alijenga hapo hekalu lake kubwa kama mbingu, kama dunia aliyoiimarisha milele. Alimuchagua Daudi, mutumishi wake, akamutoa katika kazi ya kuchunga kondoo. Alimutoa katika kazi ya kuchunga kondoo na wana-kondoo, akuwe na madaraka ya kuchunga watu wa Yakobo taifa lake, achunge Israeli, watu wa pekee wa Mungu. Daudi akawafundisha kwa moyo mukamilifu, akawaongoza kwa uhodari mukubwa. Zaburi ya Asafu. Ee Mungu, watu wasiokujua wameshambulia inchi yako. Wamechafua hekalu lako takatifu, wameugeuza Yerusalema kuwa mabomoko. Wameacha maiti za watumishi wako zikuliwe na ndege, wametoa miili ya watu wako kwa wanyama wa pori. Damu yao imemwangwa kama maji katika Yerusalema, wamelazwa humo, wala hakuna wa kuwazika. Tunazarauliwa na mataifa jirani, jirani zetu wanatuchekelea na kutusimanga. Ee Yawe, utakasirika hata milele? Hasira yako itawaka kama moto hata wakati gani? Uyamwangie mataifa yasiyokujua hasira yako, ndizo, tawala zote zisizoheshimu jina lako. Maana wamemeza wazao wa Yakobo, wameteketeza kabisa makao ya taifa lako. Usituazibu kwa sababu ya makosa ya babu zetu. Huruma yako itufikie haraka, maana tumegandamizwa sana! Utusaidie, ee Mungu, mwokozi wetu kwa utukufu wa jina lako. Utuokoe na kutusamehe zambi zetu, kwa ajili ya jina lako. Kwa nini mataifa yatuambie: “Mungu wenu yuko wapi?” Utujalie tuone jinsi utakavyowalipiza mataifa kisasi kwa ajili ya mauaji ya watumishi wako. Kilio cha hao wafungwa kikufikie; kwa nguvu yako kubwa uwaokoe waliohukumiwa kufa. Ee Bwana, uwalipize mataifa jirani mara saba kwa ajili ya matusi waliyokutukana. Nasi watu wako, sisi kondoo wa kundi lako, tutakushukuru milele, na kukusifu nyakati zote. Kwa mukubwa wa waimbaji. Kwa mutindo wa wimbo. Zaburi ya Asafu. Unitegee sikio, ewe Muchungaji wa Israeli, unayewaongoza wazao wa Yosefu kama kondoo. Ewe unayekaa juu ya makerubi, uangaze, mbele ya kabila la Efuraimu, la Benjamina na la Manase. Uonyeshe nguvu yako, ukuje kutuokoa! Utengeneze tena maisha yetu, ee Mungu; utuangalie kwa wema, nasi tutaokoka. Ee Yawe, Mungu wa majeshi, mpaka wakati gani utakasirikia maombi ya watu wako? Umefanya huzuni ikuwe chakula chetu; umetukunywesha machozi kwa wingi. Umetufanya jambo la mazarau kwa jirani zetu; waadui zetu wanatuchekelea. Ee Mungu wa majeshi, utengeneze tena maisha yetu, utuangalie kwa wema, nasi tutaokoka. Uliongoa muzabibu kutoka Misri; ukawafukuza watu wa mataifa, na kuupandikiza katika inchi yao. Uliupalilia upate kukomaa, nao ukatoa mizizi na kuenea katika inchi yote. Uliifunika milima kwa kivuli chake, na matawi yake yakakuwa kama mierezi mikubwa. Matawi yake yalienea mpaka kwa bahari; navyo vichipukizi vyake mpaka kando ya muto Furati. Mbona ulibomoa kuta zilizouzunguka? Sasa kila anayepita anachuma zabibu zake; nguruwe wa mwitu wanauharibu, na wanyama wa pori wanautafuna! Utugeukie tena, ee Mungu wa majeshi. Uangalie toka mbinguni, uone; uutunze muzabibu huu. Ulinde kijiti ulichokipanda kwa mukono wako; hicho kichipukizi ulichokomalisha wewe mwenyewe. Watu walikikata na kukiteketeza, uwaangalie kwa ukali, waangamie. Mukono wako umukinge huyo uliyemurehemu; huyo uliyemuchagua kwa ajili yako. Hatutakuacha tena; utujalie uzima, nasi tutakusifu. Ee Yawe, Mungu wa majeshi, utengeneze tena maisha yetu; utuangalie kwa wema, nasi tutaokoka. Kwa mukubwa wa waimbaji: kwa mutindo wa watu wa Gati. Zaburi ya Asafu. Mumwimbie Mungu kwa sauti, maana ni nguvu yetu, mumushangilie Mungu wa Yakobo, muvumishe wimbo wa shangwe, mupige ngoma, mucheze zeze na kinubi cha sauti nzuri. Mupige baragumu kutangaza mwandamo wa mwezi, na pia mbalamwezi wakati wa sikukuu yetu. Hilo ndilo sharti katika Israeli; hilo ndilo agizo la Mungu wa Yakobo. Aliwapa watu wa Israeli agizo hilo, aliposhambulia inchi ya Misri. Ninasikia sauti nisiyoitambua ikisema: “Mimi nilikutua mizigo yako toka kwenye mabega, nilikuondolea matofali uliyochukua katika mikono. Katika shida uliniita, nami nikakuokoa. Nilikujibu kutokea katika ngurumo. Nilikujaribu kwenye maji ya Meriba. Enyi watu wangu, musikie onyo langu. Heri ungenisikiliza, ee Israeli! Usikuwe na mungu wa kigeni; usiabudu hata kidogo mungu mwingine. Mimi ni Yawe, Mungu wako, niliyekutoa katika inchi ya Misri. Fungua kinywa chako, nami nitakulisha. “Lakini watu wangu hawakunisikiliza; Israeli hakunitaka kabisa. Hivyo, nikawaacha wabaki katika ugumu; wafuate mashauri yao wenyewe. Heri watu wangu wangenisikiliza! Heri Israeli angefuata njia zangu! Ningewashinda waadui zao haraka; ningenyoosha mukono juu ya wapinzani wao. Wanaonichukia wangenipigia magoti kwa hofu, na azabu yao ingekuwa ya milele. Lakini wewe ningekulisha kwa ngano bora, ningekushibisha kwa asali ya pori.” Zaburi ya Asafu. Mungu anasimamia baraza lake. Anatoa hukumu katika kusanyiko la miungu: “Mpaka wakati gani mutaendelea kuhukumu bila haki na kuwapendelea watu waovu? Muimarishe sheria yangu kwa wazaifu na wayatima; muwatendee wasiojiweza na wamasikini kwa haki. Muwaokoe wazaifu na wakosefu, muwaopoe kutoka makucha ya waovu. “Lakini ninyi hamujui wala hamufahamu! Ninyi munatembea katika giza la upotovu! Misingi yote ya haki katika dunia imetikiswa! Mimi nilisema kwamba ninyi ni miungu, kwamba ninyi wote ni wana wa Mungu Mukubwa! Hata hivyo, mutakufa kama watu wote; mutaanguka kama mukubwa yeyote.” Simama sasa, ee Mungu, uuhukumu ulimwengu; maana mataifa yote ni mali yako. Zaburi ya Asafu. Wimbo. Ee Mungu, usikae kimya! Usinyamaze, ee Mungu, wala usitulie! Angalia! Waadui zako wanafanya fujo; wanaokuchukia wanainua vichwa kwa kiburi. Wanafanya mipango mibaya kwa kuwazuru watu wako; wanashauriana juu ya hao unaowalinda. Wanasema: “Mukuje tuangamize taifa lao, hata jina la Israeli lisikumbukwe tena.” Kweli, wanakubaliana kwa moyo moja, wanafanya mapatano juu yako: Waedomu na Waisimaeli, Wamoabu na Wahagari; Wagebali, Waamoni na Waamaleki, Wafilistini na wakaaji wa Tiro. Hata Waasuria wameshirikiana nao, wamewaunga mukono wazao wa Loti! Uwatendee ulivyowatendea Wamidiani, ulivyowatendea Sisera na Mufalme Asikie kwenye muto Kisoni, watu uliowaangamiza kule Endori, wakakuwa takataka juu ya inchi. Uwatendee wakubwa na watawala wao kama Kibombobombo na Mbwa wa Pori, kama Sadaka na Kivuli, ambao walisema: “Tutajitwalia inchi ya Mungu.” Ee Mungu wangu, uwafanye kama mavumbi; kama makapi yanayopeperushwa na upepo. Kama vile moto unavyoteketeza pori, na ndimi za moto zinavyounguza milima, uwakimbize hao kwa zoruba yako, na kuwatisha kwa upepo wako mukali! Ujaze nyuso zao haya, wapate kukutafuta, ee Yawe. Wafezeheke na kuhangaika milele, waangamie kwa haya kabisa. Wajue kwamba wewe peke yako, ambaye jina lako ni Yawe, ndiwe Mungu Mukubwa juu ya dunia yote. Kwa mukubwa wa waimbaji: kwa mutindo wa watu wa Gati: Zaburi ya Wakora. Ee Yawe wa majeshi, kweli makao yako yanapendeza! Nafsi yangu inatamani sana hekalu la Yawe! Moyo na mwili wangu wote vinamushangilia Mungu Mwenye Uzima. Karibu na mazabahu zako, ee Yawe wa majeshi, mufalme wangu na Mungu wangu, hata kichororo ana makao yake, naye mbaruwayi amejenga chicha yake ambamo anaweka vitoto vyake, Heri wale wanaokaa ndani ya nyumba yako, wakiimba sifa zako siku zote. Heri watu wanaopata nguvu zao kwako, wanaotamani kusafiri kwa kuabudu kwa mulima wako. Wanapopita katika bonde lenye kukauka la Baka, wanalifanya kuwa chemichemi, nazo mvua za kwanza zinalijaza maji. Wanaendelea wakipata nguvu zaidi na zaidi: watamwona Mungu wa miungu huko Sayuni. Usikie maombi yangu, ee Yawe, Mungu wa majeshi! Unitegee sikio, ee Mungu wa Yakobo. Ee Mungu, umwangalie huyo ngao yetu, upendezwe na huyo uliyemuchagua. Siku moja tu ndani ya hekalu lako, ni bora kuliko siku elfu pahali pengine; afazali kubakia kwa mulango wa nyumba yako, kuliko kuishi ndani ya nyumba ya waovu. Yawe Mungu ni jua na ngao yetu. Anatukubali na anatupatia utukufu. Hawanyimi kitu chochote kizuri wale wanaoishi katika ukamilifu. Ee Yawe wa majeshi, heri mutu yule anayekutumainia wewe! Kwa mukubwa wa waimbaji: Zaburi ya Wakora. Ee Yawe, umependelea inchi yako; umerudishia wazao wa Yakobo hali nzuri. Umewasamehe watu wako kosa lao; umefuta zambi zao zote. Umezuia kasirani yako yote; umeacha hasira yako kali. Utustareheshe tena, ee Mungu mwokozi wetu; uondoe chuki unayokuwa nayo juu yetu. Utatukasirikia hata milele? Utadumisha kasirani yako kwa vizazi vyote? Hautatujalia tena maisha mapya, kusudi watu wako wafurahi kwa sababu yako? Utuonyeshe wema wako, ee Yawe, utujalie wokovu wako. Ninasikiliza yale Yawe anayosema, maana anaahidi kuwapa watu wake amani, watu wake mwenyewe wasiporudilia upumbafu wao. Hakika yeye ni tayari kuwaokoa wanaomuheshimu, na utukufu wake utadumu katika inchi yetu. Wema na uaminifu vitakutana; haki na amani vitashikamana. Uaminifu utachipuka katika inchi; haki utashuka toka mbinguni. Kweli, Yawe atatuletea baraka, na inchi yetu itatoa mazao yake mengi. Haki itamutangulia Mungu na kumutayarishia njia yake. Maombi ya Daudi. Unitegee sikio, ee Yawe, unijibu, maana mimi ni masikini na mukosefu. Ulinde maisha yangu maana mimi ni mwaminifu mbele yako; uniokoe mimi mutumishi wako ninayekutegemea. Wewe ni Mungu wangu; basi, unionee huruma, maana ninakulilia muchana kutwa. Ee Bwana wetu, ninakutolea moyo wangu. Ufurahishe roho yangu mimi mutumishi wako. Ee Bwana, wewe ni muzuri na mwenye kusamehe, mwingi wa wema kwa wote wanaokuomba. Ee Yawe, utegee maombi yangu sikio; usikilize kilio cha ombi langu. Siku za taabu ninakuita, maana wewe unaniitikia. Ee Bwana, hakuna mungu mwingine anayekuwa kama wewe; hakuna anayeweza kufanya unayofanya wewe. Mataifa yote uliyoumba, yatakuja kukuabudu, ee Bwana; yatatangaza ukubwa wa jina lako. Wewe ndiwe mukubwa, unafanya maajabu; wewe peke yako ndiwe Mungu. Unifundishe njia yako, ee Yawe, nipate kuwa mwaminifu kwako; uongoze moyo wangu nikuheshimu. Ee Bwana, Mungu wangu, nitakusifu kwa moyo wote; nitatangaza ukubwa wa jina lako milele. Wema wako kwangu ni mwingi sana! Umeniokoa kutoka katika kuzimu. Ee Mungu, watu wenye kiburi wamenishambulia; kundi la watu wakali lilitaka kuniua, wala halikujali wewe hata kidogo. Lakini wewe, Bwana, ni Mungu wa rehema na huruma; wewe ni muvumilivu, mwingi wa wema na uaminifu. Unigeukie, unihurumie; unijalie nguvu yako mimi mutumishi wako, umwokoe mutoto wa mujakazi wako. Unionyeshe kitambulisho cha wema wako, ee Yawe, kusudi wale wanaonichukia wafezeheke, wanapoona umenisaidia na kunifariji. Zaburi ya Wakora: Wimbo. Mungu amejenga muji wake juu ya mulima wake mutakatifu. Yawe anapenda Sayuni, kuliko makao mengine ya Yakobo. Ee muji wa Mungu, mambo ya utukufu yanasemwa juu yako. Kati ya wale wanaonijua mimi, kuna Wamisri na Wababeli. Vilevile Wafilistini, Watiro na Waetiopia. Wanasema: “Huyu amezaliwa kule.” Lakini juu ya Sayuni itasemwa: “Sayuni ni mama yao wote; Mungu Mukubwa atauimarisha.” Yawe atakapohesabu watu, ataandika hivi katika kitabu: “Huyu amezaliwa kule!” Wote wanacheza ngoma na kuimba: “Sayuni shina letu ni kwako.” Kwa mukubwa wa waimbaji. Zaburi ya Wakora: Kwa mutindo wa wimbo wa huzuni. Mashairi ya Hemani Mwezra. Ee Yawe, mwokozi wangu, ninalia muchana kutwa, na usiku ninakulalamikia. Maombi yangu yakufikie, usikilize kilio changu. Hasara inanipita kipimo, nami niko karibu kufa. Ninaonekana kama mutu anayeshuka katika shimo la wafu. Nguvu zangu zote zimeniishia. Ninahesabiwa kati ya wafu, kama waliouawa, wanaokuwa katika kaburi, kama wale ambao hauwakumbuki tena, ambao wametengwa na ulinzi wako. Umenitupa mbali katika shimo la wafu, katika giza kubwa. Hasira yako imenilemea; umenisonga kwa zoruba yako yote. Umewafanya warafiki zangu waniepuke, umenifanya kuwa chukizo kwao. Nimefungwa wala siwezi kutoroka. Macho yangu yamefifia kwa huzuni. Kila siku ninakulilia, ee Yawe. Ninakunyooshea mikono yangu. Wewe unawatendea wafu maajabu yako? Waliokufa wanafufuka na kukusifu? Wema wako unatajwa ndani ya kaburi, au uaminifu wako katika shimo la kuangamia? Maajabu yako yanajulikana humo katika giza, au matendo yako ya haki katika inchi ya waliosahauliwa? Mimi ninakulilia, ee Yawe. Kila asubui ninakuletea ombi langu. Mbona, ee Yawe, unanitupilia mbali? Kwa nini unanificha uso wako? Nimeteseka na kukaribia kifo tangu ujana wangu; ninateseka kwa mapigo yako, niko tabani kabisa. Kasirani yako imeniwakia; mashambulio yako ya kutisha yananiangamiza. Yananizunguka kama mafuriko muchana kutwa; yananizunguka yote pamoja. Umewafanya warafiki na wenzangu wote waniepuke; giza ndilo limekuwa mwenzangu. Mashairi ya Etani, Mwezra. Ee Yawe, nitayaimba mema yako kwa milele; nitatangaza uaminifu wako kwa vizazi vyote. Nitasema kwamba wema wako unadumu kwa milele, uaminifu wako ni imara kama mbingu. Wewe umesema: “Nimefanya agano na muchaguliwa wangu, nimemwapia mutumishi wangu Daudi hivi: ‘Siku zote nitamuweka mumoja wa wazao wako kuwa mufalme, tena nitaudumisha ufalme wako milele.’ ” Ee Yawe, mbingu zinasifia maajabu yako, uaminifu wako unasifiwa katika kusanyiko la watakatifu. Nani katika mbingu anayeweza kulinganishwa nawe, ee Yawe? Nani anayekuwa sawa nawe kati ya miungu? Wewe unatisha katika baraza la watakatifu; wote wanaokusanyika mbele yako wanakuheshimu na kukuogopa. Ee Yawe, Mungu wa majeshi, ni nani mwenye nguvu kama wewe? Ee Yawe, uaminifu umekuzunguka pande zote. Wewe unaamuru machafuko ya bahari; mawimbi yake yakiinuka, unayatuliza. Ulimuponda nyama mukubwa Rahaba na kumwua; uliwatawanya waadui zako kwa nguvu yako. Mbingu ni zako na dunia ni yako pia; ni wewe uliyeumba ulimwengu na vyote vinavyokuwa ndani yake. Wewe uliumba kaskazini na kusini; milima Tabori na Hermoni inakushangilia. Mukono wako unajaa nguvu, mukono wako una nguvu na umeshinda! Haki na sheria ndio musingi wa utawala wako; wema na uaminifu vinakutangulia! Heri watu wanaojua kukushangilia, wanaoishi katika mwangaza wa wema wako, ee Yawe. Wanafurahi muchana kutwa kwa sababu yako, na kukusifu kwa ajili ya haki yako. Wewe ndiwe utukufu na nguvu yao; kwa upendo wako tunapata ushindi. Ee Yawe, ngao yetu ni chini ya ulinzi wako. Mufalme wetu ametoka kwako, ewe Mutakatifu wa Israeli. Zamani ulisema katika maono, ukawaambia watumishi wako waaminifu: “Nimemupa nguvu shujaa mumoja, nimemwinua huyo niliyemuchagua kati ya watu. Nimemupata mutumishi wangu Daudi; nimemuchagua kwa kumupakaa mafuta yangu matakatifu. Mukono wangu wa nguvu utakuwa naye siku zote; mukono wangu mimi mwenyewe utamwimarisha. Waadui hawataweza kumushinda, wala waovu hawatamwonea. Mimi nitawaponda wapinzani wake; nitawaangamiza wote wanaomuchukia. Nitakuwa mwaminifu na mwema kwake. Kwa jina langu atapata ushindi mukubwa. Nitaongeza nguvu na utawala wake, kutoka bahari ya Mediteranea mpaka muto Furati. Yeye atasema, ‘Wewe ni baba yangu, Mungu wangu, mulima wa wokovu wangu.’ Nami nitamufanya kuwa muzaliwa wangu wa kwanza, mukubwa kuliko wafalme wote wa dunia. Nitamwonyesha wema wangu kwa milele, na agano langu kwake litadumu siku zote. Nitaudumisha ukoo wake wa kifalme siku zote, nao ufalme wake kama mbingu. “Lakini wazao wake wakiiacha sheria yangu, wasipoishi kufuatana na maagizo yangu, kama wakivunja masharti yangu, na kuacha kutii amri zangu, hapo nitayaazibu makosa yao; nitawapiga kwa sababu ya maovu yao. Lakini sitaacha kumutendea mema Daudi, wala sitavunja uaminifu wangu kwake. Sitavunja agano langu naye, wala kugeuza neno nililosema kwa mudomo wangu. “Nimeapa mara moja tu kwa utakatifu wangu; nami sitamwambia Daudi uongo. Ukoo wake utadumu milele, nao ufalme wake kama jua. Utadumu milele kama mwezi unaokuwa mushuhuda mwaminifu asiyetoka katika anga.” Lakini sasa, ee Mungu, umemutupa na kumukataa, umejaa kasirani juu ya huyo uliyemuchagua. Umefuta agano ulilofanya na mutumishi wako; umeitupa taji yake ya kifalme ndani ya mavumbi. Umebomoa kuta zote za muji wake; umezivunjavunja nafasi zake za kukimbilia. Wote wanaopita wanaiba mali zake; wajirani zake wanamuzarau. Umewapatia waadui ushindi; umewafurahisha waadui zake wote. Umepoteza ukali wa silaha zake; ukamwachilia ashindwe katika vita. Umemuvua madaraka yake ya kifalme, ukauangusha utawala wake chini. Umezipunguza siku za ujana wake, ukamufunika haya tele. Ee Yawe, utajificha hata milele? Mpaka wakati gani hasira yako itawaka kama moto? Unikumbuke, ee Bwana. Maisha ni mafupi! Umewaumba wanadamu wote kwa bure? Ni mutu gani anayeweza kuishi pasipo kufa? Nani anayeweza kujiepusha na kifo? Ee Bwana, yako wapi yale mema yako ya zamani uliyomwahidi Daudi kwa uaminifu wako? Ee Bwana, ukumbuke matusi ya mutumishi wako, jinsi ninavyovumilia mazarau ya mataifa. Ee Yawe, ona jinsi wanavyomuzomea muchaguliwa wako. Wanamuzomea kila fasi anapokwenda. Yawe asifiwe milele! Amina! Amina! Maombi ya Musa, mutu wa Mungu. Ee Bwana, tangia vizazi vyote, wewe umekuwa usalama wetu. Mbele milima haijakuwa, mbele haujauumba ulimwengu, wewe ndiwe Mungu, milele na milele. Unawarudisha watu katika mavumbi walimotoka, ukisema: “Wanadamu, murudi!” Kwako miaka elfu moja ni kama siku moja tu, ni kama jana ambayo imekwisha pita, ni kama makesha ya usiku mumoja. Unatowesha mbali watu kama ndoto! Wanadamu ni kama majani yanayochipuka asubui: asubui yanachipuka na kuchanua, magaribi yamekwisha nyauka na kukauka. Hasira yako inatuangamiza; tunatishwa na kasirani yako. Maovu yetu umeyaweka mbele yako; zambi zetu za siri ziko wazi mbele yako. Kwa hasira yako maisha yetu yanatoweka, yanaisha kama pumzi. Muda wa maisha yetu ni miaka makumi saba, au tukikuwa wenye afya, miaka makumi nane; lakini yote ni shida na taabu! Siku zinapita mbio, nasi tunatoweka! Nani anayetambua uzito wa hasira yako? Nani anayeona matokeo ya kasirani yako? Utufundishe ufupi wa maisha yetu kusudi tuweze kuwa na hekima. Ee Yawe, urudie! Utakasirika mpaka wakati gani? Utuonee huruma sisi watumishi wako. Utushibishe wema wako kila asubui, tupate kushangilia na kufurahi maisha yetu yote. Utujalie sasa miaka mingi ya furaha, kama ulivyotupa miaka mingi ya shida na taabu. Utuonyeshe matendo yako sisi watumishi wako; uwaonyeshe wazao wetu utukufu wako. Utuonyeshe uzuri wako, ee Bwana, Mungu wetu; uimarishe kazi zetu, uziimarishe. Ukikaa chini ya ulinzi wa Mungu Mukubwa, ukiishi chini ya kivuli cha Mungu Mwenye Nguvu, utaweza kumwambia Yawe: “Wewe ni kimbilio langu ninamojificha, Mungu wangu ninayemutumainia!” Hakika Mungu atakuokoa katika mutego, atakukinga na magonjwa mabaya. Atakufunika kwa mabawa yake; utapata usalama kwake. Uaminifu wake ni ngao ya kukinga. Hautaogopa vitisho vya usiku, wala shambulio la rafla muchana. Hautaogopa ugonjwa mukali unaotokea usiku, wala hasara inayotokea muchana. Kama watu elfu wakianguka pembeni yako, hata elfu kumi karibu yako, hasara haitakupata. Kwa macho yako mwenyewe utaangalia, na kuona jinsi watu waovu wanavyoazibiwa. Wewe umemufanya Yawe kuwa kimbilio lako; Mungu anayekuwa juu kuwa tegemeo lako. Kwa hiyo, hautapatwa na hasara yoyote; nyumba yako haitakaribiwa na pigo lolote. Maana Mungu atawaamuru wamalaika wake, wakulinde popote unapoenda. Watakuchukua katika mikono yao, kusudi usijikwae kwenye jiwe. Utakanyaga simba na nyoka wa hatari, utawaponda simba wakali na nyoka. Mungu anasema: “Nitamwokoa yule anayenipenda; nitamulinda anayejua jina langu! Akiniita, mimi nitamwitikia; akikuwa katika taabu nitakuwa pamoja naye, nitamwokoa na kumupa heshima. Nitamupa maisha marefu, nitamujalia wokovu wangu.” Zaburi. Wimbo wa Siku ya Sabato. Ni vizuri kukushukuru, ee Yawe, kuliimbia jina lako sifa, ee Mungu Mukubwa. Ni vizuri kutangaza wema wako asubui, na uaminifu wako kwa wakati wa usiku, kwa muziki wa zeze na kinubi, kwa sauti tamu ya zeze. Ee Yawe, matendo yako makubwa yananifurahisha; nitashangilia kwa sababu ya mambo yote uliyotenda. Matendo yako, ee Yawe, ni makubwa sana! Mawazo yako hayatambulikani! Mutu mupumbafu hawezi kufahamu, wala mujinga hajui jambo hili: kwamba waovu wanaweza kustawi kama majani, watenda maovu wote wanaweza kufanikiwa, lakini mwisho wao ni kuangamia milele. Lakini wewe, ee Yawe, ni mukubwa kwa milele. Hao waadui zako, ee Yawe, hao waadui zako, hakika wataangamia; wote wanaotenda maovu, watatawanyika! Wewe umenipa nguvu kama mbogo; umenimimia mafuta kwa kunifurahia. Kwa macho yangu, nimeona waadui zangu wameshindwa; kwa masikio yangu, nimesikia kilio cha wanaotenda maovu. Watu wa haki wanastawi kama mingazi; wanakomaa kama mierezi ya Lebanoni! Kama miti iliyopandwa katika nyumba ya Yawe, wanastawi katika viwanja vya Mungu wetu; inaendelea kuzaa matunda hata katika uzee; siku zote wamejaa utomvu na wabichi, wapate kutangaza kwamba Yawe ni wa usawa. Yeye ni kikingio changu. Kwake hakuna upotovu. Yawe anatawala; amejifunika utukufu mukubwa! Yawe amevaa utukufu na nguvu! Ameimarisha ulimwengu, hautatikisika hata kidogo. Kiti chako cha kifalme ni imara tangu zamani; wewe umekuwa mbele ya nyakati zote. Ee Yawe, bahari zimetoa sauti; zimenyanyua sauti zao, bahari zinanyanyua tena uvumi wao. Yawe ana mamlaka juu mbinguni, ana nguvu kuliko mulio wa bahari, ana nguvu kuliko mawimbi ya maji. Ee Yawe, maagizo yako ni imara; nyumba yako ni takatifu milele. Ee Yawe, Mungu mwenye kulipiza kisasi, ewe Mungu mwenye kulipiza kisasi, ujitokeze! Usimame, ee mwamuzi wa watu wote; uwaazibu wenye kiburi inavyowastahili! Waovu wataona utukufu mpaka wakati gani? Watajisifia mpaka wakati gani, ee Yawe? Mpaka wakati gani waovu watajigamba kwa maneno? Watajivuna na kujitapa mpaka wakati gani? Wanaangamiza watu wako, ee Yawe, wanawagandamiza hao wanaokuwa mali yako. Wanaua wajane na wageni; wanachinja wayatima. Wanasema: “Yawe haoni, Mungu wa Yakobo hajui.” Enyi wajinga wa mwisho, mufikiri kidogo! Enyi wapumbafu, mutapata akili wakati gani? Aliyefanya sikio, yeye hawezi kusikia? Aliyeumba jicho, yeye hawezi kuona? Mwenye kuonya mataifa, yeye hawezi kuazibu? Mwenye kufundisha wanadamu, yeye hana akili? Yawe anajua mawazo ya watu; anajua kwamba hayafai kitu. Heri mutu unayemwadibisha, ee Yawe, mutu unayefundisha sheria yako, kusudi siku ya taabu apate utulivu, mpaka waovu wachimbiwe shimo. Yawe hatawaachilia watu wake; hatawatupa hao wanaokuwa mali yake. Maana hukumu zitatolewa kwa haki tena, na wote wenye moyo wa usawa watazifuata. Nani aliyenisaidia kumupinga mutu mwovu? Nani aliyekuwa upande wangu juu ya wabaya? Yawe asingalinisaidia, ningalikwisha kwenda kwenye inchi ya wafu. Nilipotambua kwamba ninateleza, wema wako, ee Yawe, ulinikingia. Mahangaiko ya moyo wangu yanapozidi, wewe unanifariji na kunifurahisha. Wewe hauwezi kushirikiana na waamuzi wapotovu, wanaotunga masharti za kutetea maovu. Wao wanapatana kuwaangamiza watu wa haki, na kuwahukumu watu wasiokuwa na kosa wauawe. Lakini Yawe ni kimbilio langu; Mungu wangu ni kikingio changu. Atawarudishia uovu wao wenyewe, atawateketeza kwa sababu ya ubaya wao. Yawe, Mungu wetu, atawateketeza kabisa! Mukuje tumwimbie Yawe, tumushangilie yeye kikingio na mwokozi wetu! Tuende mbele yake na nyimbo za shukrani; tumushangilie kwa nyimbo za sifa. Maana Yawe ni Mungu mukubwa; yeye ni mufalme mukubwa juu ya miungu yote. Mabonde ni katika mikono yake, vilele vya milima ni vyake. Bahari ni yake, ndiye aliyeifanya; kwa mikono yake aliumba inchi kavu. Mukuje tuiname chini na kumwabudu; tumupigie magoti Yawe, Muumba wetu! Maana yeye ni Mungu wetu. Sisi ni watu wake, kondoo wanaochungwa katika malisho yake. Heri leo mungesikiliza hivi anavyosema: “Musikuwe wagumu kama kule Meriba, kama ilivyokuwa kule Masa katika jangwa, babu zenu waliponijaribu na kunipima, ingawa walikuwa wameona mambo niliyowatendea. Kwa miaka makumi ine nilichukizwa nao, nikasema: ‘Kweli, hawa ni watu waliopotoka! Hawajali kabisa njia zangu!’ Basi, nikaapa kwa kasirani kwamba hawataingia kwenye mapumziko niliyowatayarishia.” Mumwimbie Yawe wimbo mupya! Mumwimbie Yawe, ninyi ulimwengu wote! Mumwimbie Yawe na kusifu jina lake. Mutangaze kila siku matendo yake ya wokovu. Muyatangazie mataifa utukufu wake, muwaambie watu wote matendo yake ya ajabu. Maana Yawe ni mukubwa, anasifiwa sana; anastahili kuheshimiwa kuliko miungu yote. Miungu ya mataifa si kitu; lakini Yawe ndiye aliyeumba mbingu. Heshima na sifa vinamuzunguka; nguvu na uzuri vinajaza hekalu lake. Mumupe Yawe heshima, enyi watu wa kila namna; mutangaze utukufu na nguvu yake. Mumupe Yawe utukufu wa jina lake. Mulete sadaka na kuingia katika viwanja vya hekalu lake. Mumwabudu Yawe katika pahali pake patakatifu; tetemeka mbele yake, ee dunia nzima! Muyaambie mataifa: “Yawe anatawala! Ameuweka ulimwengu imara, hautatikisika. Atahukumu mataifa kama vile inavyofaa.” Mufurahi, enyi mbingu na dunia! Bahari ivume pamoja na vyote vinavyokuwa ndani yake! Mufurahi, enyi mbuga na vyote vinavyokuwa ndani yenu! Halafu miti yote ya pori itaimba kwa furaha, mbele ya Yawe kwa sababu anakuja. Anakuja kuhukumu dunia. Atahukumu dunia kwa haki, na mataifa kwa uaminifu wake. Yawe anatawala! Furahi, ee dunia! Mufurahi, enyi visanga vingi! Mawingu na giza nzito vinamuzunguka; haki na sheria ni musingi wa utawala wake. Moto unatangulia mbele yake, na kuwateketeza waadui zake pande zote. Umeme wake unaangaza ulimwengu; dunia inauona na kutetemeka. Milima inayeyuka kama inta mbele ya Yawe, mbele ya Bwana wa dunia yote. Mbingu zinatangaza haki yake; na mataifa yote yanauona utukufu wake. Wote wanaoabudu sanamu na kujisifia miungu ya bure wanafezeheshwa. Miungu yote inainama mbele yake. Watu wa Sayuni wanasikia hayo na kufurahi; watu wa Yuda wanashangilia kwa ajili ya hukumu zako, ee Mungu. Wewe Yawe ni mukubwa juu ya dunia yote; wewe unatukuzwa juu ya miungu yote. Yawe anawapenda wale wanaochukia uovu, anayalinda maisha ya watu wake, anawaokoa kutoka makucha ya waovu. Mwangaza unamwangazia mutu wa haki, nayo furaha ni kwa watu wenye moyo wa usawa. Mufurahi kwa sababu ya Yawe, enyi watu wa haki; mumushukuru kwa ajili ya utakatifu wake. Zaburi. Mumwimbie Yawe wimbo mupya, kwa maana ametenda mambo ya ajabu! Nguvu yake kubwa, mukono wake mutakatifu umemupatia ushindi. Yawe ameonyesha ushindi wake; ameonyesha wazi kwa mataifa uwezo wake wa kuokoa. Amekumbuka wema na uaminifu wake kwa Waisraeli. Pande zote za dunia zimeuona ushindi wa Mungu wetu. Dunia yote imushangilie Yawe; imusifu kwa nyimbo na vigelegele. Mumusifu Yawe kwa shangwe, mumusifu kwa sauti tamu za zeze. Mumupigie vigelegele Yawe mufalme wetu, mumushangilie kwa sauti ya baragumu na ngunga. Bahari ivume na vyote vinavyokuwa ndani yake, dunia na wote wanaoishi ndani yake. Enyi mito, mupige vigelegele; enyi vilima, muimbe pamoja kwa shangwe. Mushangilie mbele ya Yawe, maana anakuja kutawala dunia. Atahukumu ulimwengu kwa haki, atatawala mataifa kama vile inavyofaa. Yawe anatawala, mataifa yanatetemeka! Ameikaa juu ya makerubi, nayo dunia inatikisika! Yawe ni mukubwa katika Sayuni; ametukuzwa kuliko mataifa yote. Wote wasifu jina lake kubwa la kutisha. Yeye ni mutakatifu! Ee mufalme mukubwa, mupenda haki, umesimamisha usawa katika Israeli; umeleta sheria na haki. Mumusifu Yawe, Mungu wetu; muiname uso mpaka chini mbele yake. Yeye ni mutakatifu! Musa na Haruni walikuwa makuhani wake; Samweli alikuwa kati ya waliomulilia. Walimulilia Yawe naye akawasikiliza. Alisema nao katika nguzo ya wingu; walitimiza maagizo yake na masharti aliyowapa. Ee Yawe, Mungu wetu, wewe uliwasikiliza; ulikuwa kwao Mungu mwenye kusamehe, ingawa uliwaazibu kwa makosa yao. Mumusifu Yawe, Mungu wetu; muiname kwa mulima wake mutakatifu! Yawe, Mungu wetu, ni mutakatifu. Zaburi ya shukrani. Mumushangilie Yawe, enyi inchi zote! Mumwabudu Yawe kwa furaha, mukuje mbele yake mukiimba kwa shangwe! Mujue kwamba Yawe ndiye Mungu. Yeye ndiye aliyetuumba, sisi ni mali yake; sisi ni watu wake na kondoo wake anaowachunga. Muingie ndani ya hekalu lake kwa shukrani, muingie katika kiwanja chake kwa kumusifu. Mumushukuru na kulisifu jina lake. Yawe ni muzuri! Wema wake unadumu milele, na uaminifu wake kwa vizazi vyote. Zaburi ya Daudi. Wimbo wangu unaelekea wema na haki; ninauimba kwa heshima yako, ee Yawe. Nitashikamana na mwenendo mukamilifu. Utakuja kwangu wakati gani? Nitaishi kwa ukamilifu ndani ya nyumba yangu; sitavumilia hata kidogo mambo ya upuuzi. Ninachukia matendo ya watu wapotovu, mimi sitaambatana nayo. Upotovu wowote ukuwe mbali nami; sitahusika kabisa na uovu. Nitateketeza yule anayemuteta mwenzake, sitamuvumilia mwenye majivuno na kiburi. Nitawaangalia waaminifu katika inchi, wapate kuishi pamoja nami. Watu wakamilifu, ndio watakaonitumikia. Mwongo yeyote hatakaa ndani ya nyumba yangu; hakuna musema uongo atakayekaa kwangu. Siku kwa siku nitawaangamiza waovu wote katika inchi; nitawaangamiza wabaya wote katika muji wa Yawe. Maombi ya mutu anayekuwa katika taabu ambaye anamutolea Yawe malalamiko yake. Ee Yawe, usikie maombi yangu, na kilio changu kikufikie. Usijifiche mbali nami wakati wa taabu! Unitegee sikio lako, unijibu upesi wakati ninapokuomba! Siku zangu zinapita kama moshi; mifupa yangu inaungua kama katika furu. Nimepondekana kama majani na kunyauka; sina hata hamu ya chakula. Kutokana na kuugua kwangu, nimebaki mifupa na ngozi. Nimekuwa kama ndege katika jangwa, kama bundi kwenye matongo. Ninalala macho wazi, kama ndege anayekuwa peke yake juu ya paa. Muchana kutwa waadui zangu wananisimanga, wanaonichekelea wanatumia jina langu kwa kulaani. Majivu yamekuwa chakula changu, machozi yanachangana na kinywaji changu, kwa sababu ya kasirani na hasira yako, maana umeniokota na kunitupilia mbali. Maisha yangu ni kama kivuli cha magaribi; ninanyauka kama majani. Lakini wewe, ee Yawe, unatawala milele; jina lako linakumbukwa katika vizazi vyote. Wewe utasimama na kurehemu Sayuni, maana wakati umefika wa kuuhurumia, wakati wake uliopangwa umefika. Watumishi wako wanapenda muji ule, ijapokuwa ni mabomoko sasa; wanauonea huruma, ingawa umeharibika kabisa. Mataifa yataheshimu jina la Yawe; wafalme wote katika dunia wataogopa utukufu wake. Yawe atajenga upya Sayuni, na kuonyesha utukufu wake. Atakubali maombi ya mukosefu; wala hatakataa maombi yao. Andika jambo hili kwa ajili ya vizazi vinavyokuja kusudi watakaozaliwa kisha wamusifu Yawe, kwamba alichungulia chini kutoka katika pahali pake patakatifu. Yawe aliangalia dunia kutoka mbinguni, akasikia malalamiko ya wafungwa, akawaachilia huru waliohukumiwa kuuawa. Watu watatangaza jina la Yawe kule Sayuni; sifa zake zitatangazwa kule Yerusalema, wakati mataifa yatakapokusanyika pamoja na falme zitakapokutana kumwabudu Yawe. Mungu amenipunguzia nguvu ningali kijana; amefupisha maisha yangu. Ee Mungu wangu, usinihamishe sasa wakati ningali bado kijana. Ee Yawe, wewe unadumu milele. Wewe uliumba dunia tokea zamani, mbingu ni kazi ya mikono yako. Vitatoweka na kuchakaa kama nguo, lakini wewe utabaki. Utavibadilisha kama nguo, navyo vitapita. Lakini wewe unabaki sawasawa, na maisha yako hayana mwisho. Watoto wa watumishi wako watakaa salama; wazao wao wataimarishwa mbele yako. Zaburi ya Daudi. Ee nafsi yangu, umusifu Yawe; nafsi yangu yote isifu jina lake takatifu! Ee nafsi yangu, umusifu Yawe! Usisahau hata kidogo matendo mazuri yake yote. Ananisamehe uovu wangu wote, na kuniponyesha magonjwa yote. Ananiokoa kutoka kifo, na kunijalia wema na rehema zake. Anajaza maisha yangu na raha, hata ninabaki kijana mwenye nguvu kama tai. Yawe anahukumu kwa haki; anawajalia wanaoteswa haki zao. Alimujulisha Musa njia zake, aliwaonyesha watu wa Israeli matendo yake makubwa. Yawe ni mwenye rehema na huruma; ni muvumilivu na mwingi wa wema. Hatukaripii siku zote, wala hasira yake haidumu milele. Yeye hatuazibu kama tunavyostahili; hatulipizi kadiri ya uovu wetu. Kama vile anga linavyokuwa juu mbali na dunia, ndivyo kipimo cha wema wake kinavyokuwa kwa watu wanaomwabudu. Kama mashariki inavyokuwa mbali na magaribi, ndivyo anavyotenga zambi zetu mbali nasi. Kama vile baba anavyohurumia mwana wake, ndivyo Yawe anavyohurumia wote wanaomwabudu. Mungu anajua jinsi tulivyoumbwa; anajua kwamba sisi ni mavumbi. Maisha ya mwanadamu ni kama majani tu, yanachanua kama maua: upepo unapovuma juu yake yanatoweka, na mahali yalipokuwa hapaonekani tena. Lakini wema wa Yawe unadumu milele, kwa wale wote wanaomwabudu; na haki yake inadumu vizazi vyote, kwa wote wanaoshika agano lake, wanaokumbuka kutii amri zake. Yawe ameweka kiti chake cha kifalme mbinguni; yeye anatawala juu ya vitu vyote. Mumusifu Yawe, enyi wamalaika wakubwa, enyi munaotimiza amri zake na kutimiza neno lake! Mumusifu Yawe, enyi kundi lote la mbinguni, enyi watumishi wake munaotimiza mapenzi yake! Mumusifu Yawe, enyi viumbe vyake vyote; mumusifu popote munapokuwa katika utawala wake. Ee nafsi yangu, umusifu Yawe! Umusifu Yawe, ee nafsi yangu! Ee Yawe, Mungu wangu, wewe ni mukubwa kabisa! Umevaa utukufu na mamlaka. Umejifunika mwangaza kama kanzu, umekunjua mbingu kama hema; umejenga makao yako katika mbingu juu ya maji. Umeyafanya mawingu kuwa gari lako nawe unatembea katika anga. Unaufanya upepo kuwa mujumbe wako, moto na ndimi zake kuwa watumishi wako. Umeiweka dunia imara juu ya misingi yake, isitikisike hata milele. Uliifunika dunia kwa bahari kama nguo, na maji yakaimeza milima mirefu. Ulipoyakaripia, yalikimbia; yaliposikia ngurumo yako, yalitelemuka mbio. Yaliporomoka toka milima mpaka katika mabonde, mpaka pahali ulipoyatengenezea. Uliyawekea hayo maji mipaka yasiyoweza kutambuka, kusudi yasifunike tena dunia. Umetokeza chemichemi katika mabonde, na vijito vyao vinapita kati ya vilima. Hivyo vinakunywesha wanyama wote wa pori, na humo punda wa pori wanatulizia kiu chao. Ndege wanajenga chicha zao katika miti ya hapo, wanatua katika matawi yake na kuimba. Toka juu angani, unainyeshea milima mvua, nayo dunia unaishibisha kwa baraka yako. Unaotesha majani kwa ajili ya mifugo, na mimea kwa matumizi ya mwanadamu kusudi naye apate chakula chake toka udongo: apate divai ya kumuchangamusha, mafuta ya muzeituni ya kumwangarisha, na mukate wa kumupa nguvu. Miti mikubwa ya Yawe inapata maji ya kutosha; ndiyo mierezi ya Lebanoni aliyoipanda. Humo, ndege wanajenga chicha zao, korongo wanafanya makao yao katika misunobari. Milima mirefu ni makao ya mbuzi wa pori; makimbilio ya sungura wa pori ni chini ya mawe. Umeumba mwezi kwa kutupimia nyakati, nalo jua linalojua wakati wa kutua. Unaleta giza, nao usiku unaingia; nao wanyama wote wa pori wanatoka: simba wakali wananguruma wanapokosa mawindo yao, wanakungojea wewe Mungu uwape chakula chao. Jua linapopanda, wanarudi kwao, na kujipumzisha ndani ya mapango yao. Hapo mwanadamu naye anaenda kwenye kazi zake; naye anatumika mpaka magaribi. Ee Yawe, matendo yako ni mengi sana! Umeyafanya kwa hekima yote! Dunia imejaa viumbe vyako! Mbali kule kuna bahari kubwa na pana, ambamo kumejaa viumbe visivyokuwa na hesabu, viumbe vizima, vikubwa na vidogo. Mashua zinasafiri humo, na yule nyama mukubwa Leviatani uliyemwumba achezee humo. Hao wote wanakungojea wewe, uwapatie chakula chao kwa wakati wake. Wanaokota kitu chochote unachowapa; ukiwafungulia mukono, wanashiba vyakula vizuri. Ukiwageuzia mugongo, wanaogopa; ukiondoa pumzi yao, wanakufa na kurudi ndani ya mavumbi walimotoka. Ukiwapulizia pumzi yako, wanaumbwa; wewe unafanya vitu vipya katika dunia. Utukufu wa Yawe unadumu hata milele; Yawe anapendezwa na matendo yake mwenyewe. Anaiangalia dunia, nayo inatetemeka; anagusa milima, nayo inatoa moshi! Nitamwimbia Yawe maisha yangu yote; nitamusifu Mungu wangu muda wote nitakaoishi. Upendezwe na hayo mashairi yangu, ee Yawe, maana wewe ndiye furaha yangu. Wenye zambi wote waondolewe katika dunia, waovu wote wasikuwe tena! Umusifu Yawe, ee nafsi yangu! Haleluia! Mumushukuru Yawe, mutangaze ukubwa wake, mujulishe mataifa mambo aliyotenda! Mushangilie, mumwimbie Mungu sifa, mueleze matendo yake ya ajabu! Mujisifu kwa ajili ya jina lake takatifu; wanaomutafuta Yawe wafurahi. Mumutafute Yawe mwenye nguvu; mumutafute Yawe siku zote. Mukumbuke matendo ya ajabu aliyotenda, miujiza yake na hukumu alizotoa, enyi wazao wa Abrahamu mutumishi wake, enyi wazao wa Yakobo muchaguliwa wake. Yeye ndiye Yawe, Mungu wetu; hukumu zake zina nguvu katika dunia yote. Yeye anashika agano lake milele, anatimiza ahadi zake kwa vizazi elfu. Anashika agano alilofanya na Abrahamu, na ahadi aliyomwapia Isaka. Alimusimamishia Yakobo ahadi yake, akamuhakikishia agano hilo la milele. Alisema: “Nitawapa inchi ya Kanana, nayo itakuwa mali yenu wenyewe.” Watu wa Mungu walikuwa wachache tu, tena walikuwa wageni katika inchi ya Kanana. Walitangatanga kutoka taifa mpaka taifa, kutoka inchi moja mpaka inchi ingine. Lakini Mungu hakuruhusu wateswe; kwa ajili yao aliwaonya wafalme, akisema: “Musiwaguse wachaguliwa wangu; musiwazuru manabii wangu!” Mungu alileta njaa katika inchi yao, akafunga njia zao zote za kupata chakula. Lakini aliwatangulizia mutu mumoja, Yosefu aliyekuwa ameuzishwa kuwa mutumwa. Walimufunga miguu kwa minyororo, na kikomo cha chuma kwenye shingo, mpaka kile alichotabiri kilipotimia. Neno la Yawe likahakikisha kwamba alikuwa na haki. Mufalme wa Misri akaamuru afunguliwe; mutawala wa mataifa akamwachilia huru. Alimuweka kuwa musimamizi wa serikali yake, na mukubwa wa mali yake yote, awaongoze wakubwa wa serikali yake sawa anavyopenda, na kuwafundisha wazee wake hekima. Halafu Israeli akaingia katika inchi ya Misri; Yakobo akakuwa mugeni katika inchi ya Hamu. Yawe akawafanya watu wake wazae sana; akawajalia nguvu kuliko waadui zao. Aliwafanya Wamisri wawachukie watu wake, wakawatendea watumishi wake vibaya. Kisha akamutuma Musa mutumishi wake, akamutuma pamoja na Haruni muchaguliwa wake. Wakafanya maajabu ya Mungu kati ya Wamisri, na miujiza katika inchi hiyo ya Hamu. Mungu akaleta giza juu ya inchi; lakini Wamisri wakakataa kutii amri zake. Akageuza mito yao kuwa damu, akaua samaki wao wote. Vyura wakajaa juu ya inchi yao, hata katika nyumba ya mufalme. Mungu akaamuru, kukatokea makundi ya mainzi, na imbu katika inchi yote. Kwa pahali pa mvua akawatumia mvua ya mawe, na radi iliyounguza inchi yao yote; akaharibu mizabibu na miti yao ya tini; akavunja miti ya inchi yao. Mungu akaamuru, kukatokea nzige, na mapanzi maelfu yasiyohesabiwa; wakatafuna mimea yote katika inchi, wakakula mazao yao yote. Aliua wazaliwa wa kwanza katika inchi yao, ndilo chipukizi la kwanza la jamaa za Wamisri. Kisha akawaondoa watu wa Israeli katika inchi, wakikuwa na feza na zahabu; wala hakuna hata mumoja wao aliyejikwaa. Wamisri walifurahia kuondoka kwao, maana hofu iliwashika kwa sababu yao. Mungu alitandaza wingu juu ya watu wake, na moto kusudi uwaangazie usiku. Waliomba, naye akawaletea kwale, akawapa mukate kutoka mbinguni kwa wingi. Alipasua jiwe maji yakabubujika; yakatiririka katika jangwa kama muto. Alikumbuka ahadi yake takatifu aliyomupa Abrahamu mutumishi wake. Basi akawaondoa watu wake katika inchi, wachaguliwa wake wakaimba na kushangilia. Aliwapa inchi za mataifa na kuwatolea mashamba ya wenyeji, kusudi watu wake watii masharti yake, na kufuata sheria zake. Haleluia! Haleluia! Mumushukuru Yawe kwa sababu ni muzuri! Wema wake unadumu milele! Ni nani anayeweza kutaja matendo ya Yawe? Ni nani anayeweza kumusifu kama anavyostahili? Heri wale wanaofuata sheria ya Mungu, wanaotenda siku zote mambo ya haki. Unikumbuke, ee Yawe, unapowaonyesha watu wako upendo. Unisaidie wakati unapowaokoa, kusudi niweze kuona uheri wa wachaguliwa wako, nipate kushiriki katika furaha ya taifa lako, na kuona utukufu pamoja na watu wako. Tumetenda zambi sisi na babu zetu; tumetenda maovu, tumefanya mabaya. Babu zetu walipokuwa Misri, hawakujali matendo ya ajabu ya Mungu; hawakukumbuka wingi wa wema wake, lakini walimwasi kando ya bahari Nyekundu. Hata hivyo Mungu aliwaokoa kama alivyoahidi, kusudi aonyeshe nguvu yake kubwa. Alikaripia bahari Nyekundu, ikakauka; akawapitisha humo kama katika inchi kavu. Aliwaokoa katika mikono ya waliowachukia; aliwaokoa kutoka nguvu za waadui zao. Maji ya bahari yaliwafunika waadui zao; wala hapakubakia hata mumoja wao. Hapo watu wake wakaamini maneno yake, wakamwimbia nyimbo za sifa yake. Lakini bila kukawia walisahau matendo yake, wakaacha kutegemea shauri lake. Walipatwa na tamaa kubwa kule katika jangwa, wakamupima Mungu kule kwenye ukiwa. Naye akawapa kile walichoomba, lakini akaleta magonjwa makali kati yao. Kule katika kambi walimwonea Musa wivu, na Haruni, mutumishi mutakatifu wa Yawe. Halafu udongo ukafunguka ukamumeza Datani, na kumuzika Abiramu na kundi lake lote; moto ukawatokea wafuasi wao, ukawateketeza watu hao waovu. Walitengeneza mwana-ngombe wa zahabu kule Horebu, wakaabudu sanamu hiyo ya chuma; walibadilisha utukufu wa Mungu kwa sanamu ya nyama ambaye anakula majani. Walimusahau Mungu aliyewaokoa, aliyetenda mambo makubwa katika inchi ya Misri, maajabu katika inchi hiyo ya Hamu, na mambo ya kutisha katika bahari Nyekundu. Mungu alisema atawaangamiza watu wake, lakini Musa, muchaguliwa wake, aliingilia kati, akazuia hasira yake isiwaangamize. Kisha wakazarau inchi ile ya kupendeza, kwa sababu hawakuaminia ahadi ya Mungu. Walinungunika ndani ya hema zao, wala hawakumusikiliza Yawe. Hivyo Mungu akainua mukono, akaapa kwamba atawaangamizia katika jangwa, atawatawanya wazao wao kati ya watu, na kuwasambaza katika dunia yote. Kisha wakajiunga kumwabudu Bali kule Peori, wakakula sadaka zilizotambikiwa kwa mizimu. Waliichochea hasira ya Yawe kwa matendo yao, magonjwa makali yakatokea kati yao. Lakini Finehasi akasimama kutoa malipizi, na yale magonjwa yakakoma. Jambo hilo linakumbukwa kwa heshima yake, tangu wakati huo na nyakati zote. Walimukasirikisha Mungu penye maji ya Meriba. Musa akapata taabu kwa ajili yao. Walimuletea uchungu katika roho, hata akasema maneno bila kufikiri. Hawakuwaua watu wa mataifa kama vile Yawe alivyowaamuru. Lakini walichanganyika na watu wa mataifa, wakajifunza kutenda mambo yao. Waliabudu sanamu za miungu yao, nazo zikakuwa mutego wa kuwaangamiza. Waliua watoto wao wanaume na wabinti, wakawatoa sadaka kwa mapepo. Walimwanga damu ya wasiokuwa na kosa, damu ya watoto wao wanaume na wabinti ambao waliwatoa sadaka kwa sanamu za Wakanana, nayo inchi ikachafuliwa kwa uuaji huo. Hivyo wakajichafua kwa matendo yao, wakakosa uaminifu kwa Mungu kama wazini. Hasira ya Yawe ikawawakia watu wake, akachukizwa sana na hao waliokuwa mali yake. Akawatoa katika mikono ya watu wa mataifa, hao wenye kuwachukia, wakawatawala. Waadui zao waliwagandamiza, wakawatumikisha kwa nguvu. Mara nyingi Mungu aliwaokoa watu wake, lakini wao wakachagua kumwasi, wakazidi kuzama katika uovu wao. Hata hivyo Mungu aliona taabu yao, wakati aliposikia kilio chao; kwa ajili yao alilikumbuka agano lake, akawahurumia kwa wingi wa wema wake. Aliwafanya wale waliowaangamiza wawaonee huruma. Utuokoe, ee Yawe, Mungu wetu, utukusanye pamoja kutoka kwa mataifa, tupate kusifu jina lako takatifu, na kuona utukufu juu ya sifa zako. Yawe, Mungu wa Israeli, asifiwe tangu milele na hata milele! Na watu wote waseme: “Amina!” Haleluia! Mumushukuru Yawe kwa sababu ni muzuri! Wema wake unadumu milele! Museme hivyo, enyi muliokombolewa na Yawe, watu ambao aliwaokoa katika taabu, akawakusanya kutoka inchi za kigeni: kutoka mashariki na magaribi, kutoka kaskazini na kusini. Wamoja walitangatanga katika jangwa tupu, hawakuweza kufikia katika muji wa kukaa. Walisikia njaa na kiu; wakavunjika moyo kabisa. Halafu katika taabu yao wakamulilia Yawe, naye akawaokoa katika mateso yao. Aliwaongoza katika njia iliyonyooka, mpaka wakafika katika muji wa kukaa. Mumushukuru Yawe kwa wema wake na maajabu yake kwa wanadamu. Yeye anakunywesha wenye kiu; na anashibisha wenye njaa mazuri. Wengine waliishi katika giza na ukiwa, wafungwa katika mateso na minyororo, kwa sababu waliasi maagizo ya Mungu, na kuzarau mashauri ya Mungu Mukubwa. Walikuwa tabani kwa kazi ngumu, wakaanguka chini, wala hawakuwa na wa kuwasaidia. Halafu katika taabu yao wakamulilia Yawe, naye akawaokoa katika mateso yao. Aliwatoa katika giza na ukiwa, na minyororo yao akaivunjavunja. Mumushukuru Yawe kwa wema wake na maajabu yake kwa wanadamu. Yeye anavunja na kufungua milango ya shaba, na kukatakata vifungio vya chuma. Wengine walipumbazika kwa sababu ya zambi zao, waliteseka kwa sababu ya uovu wao; walichukizwa na chakula, walikuwa karibu kufa. Halafu katika taabu yao wakamulilia Yawe, naye akawaokoa katika mateso yao. Kwa neno lake aliwaponyesha, akawaokoa wasiangamie. Mumushukuru Yawe kwa wema wake na maajabu yake kwa wanadamu. Wamutolee sadaka za shukrani; waeleze matendo yake kwa nyimbo za shangwe. Wengine walisafiri katika bahari ndani ya mashua, na kufanya shuguli zao humo juu ya bahari. Waliona matendo ya Yawe, mambo ya ajabu aliyotenda huko. Aliamuru, akavumisha zoruba kali, ikarusha juu mawimbi ya bahari. Walitupwa juu angani, kisha chini ndani ya shimo; uhodari wao ukawaishia katika tukio lile. Waliyumbayumba na kuwayawaya kama walevi; ufundi wao ukawaishia. Halafu katika taabu yao wakamulilia Yawe, naye akawaokoa katika mateso yao. Alituliza ile zoruba kali, nayo mawimbi yakanyamaza. Hapo wakafurahi kwa kupata utulivu; akawafikisha kwenye kivuko walichokiendea. Mumushukuru Yawe kwa wema wake na maajabu yake kwa wanadamu. Mumutukuze katika mukutano wa watu, na kumusifu katika baraza la wazee. Mungu aligeuza mito kuwa jangwa, chemichemi akazikausha kabisa. Udongo wenye mboleo akaugeuza kuwa udongo usioweza kutoa, kwa sababu ya uovu wa wakaaji wake. Aligeuza jangwa kuwa ziwa, na inchi ya kukauka kuwa chemichemi za maji. Akawahamishia wenye njaa kule, nao wakajenga muji wa kukaa humo. Walilima mashamba na kupanda mizabibu, wakavuna mazao kwa wingi. Aliwabariki watu wake, wakaongezeka; na hesabu ya wanyama wao akaizidisha. Kisha walipopunguka na kuwa wazaifu, kwa kugandamizwa, kuteswa na huzuni, aliwazarau wakubwa waliowatesa, akawazungusha katika jangwa lisilokuwa na njia. Lakini aliwaokoa wakosefu katika taabu zao, akaongeza jamaa zao kama kundi la kondoo. Watu wa usawa wanapoona jambo hilo wanafurahi, lakini waovu wote wananyamazishwa. Wenye hekima wafikiri juu ya mambo haya, watambue wema wa Yawe. Zaburi ya Daudi: Wimbo. Moyo wangu ni tayari, ee Mungu. Moyo wangu ni tayari. Nitaimba na kukushangilia! Amuka, ee nafsi yangu! Muamuke, enyi kinubi na zeze! Nitaamusha mapambazuko! Ee Yawe, nitakushukuru kati ya mataifa; nitakuimbia sifa kati ya mataifa. Wema wako ni mukubwa kuliko mbingu; uaminifu wako unaenea hata kwenye mawingu. Utukuzwe, ee Mungu, juu ya mbingu! Utukufu wako uenee katika dunia yote! Ukomboe watu hao unaowapenda; utusaidie kwa mukono wako na kutusikiliza. Mungu amesema toka hekalu lake takatifu: “Sasa nitakwenda kwa shangwe kugawanya Sekemu, bonde la Sukoti nitalipima sehemu sehemu. Gileadi ni yangu na Manase ni yangu; Efuraimu ni kofia yangu ya chuma, na Yuda ni fimbo yangu ya kifalme. Moabu ni kama bakuli langu la kunawia; nitatupia kiatu changu katika Edomu kwa kuirizi, nitapiga kelele la ushindi juu ya Wafilistini!” Ni nani atakayenipeleka katika muji unaozungukwa na kuta? Ni nani atakayeniongoza mpaka Edomu? Ee Mungu, umetuacha kabisa? Wewe hauendi tena na makundi yetu ya waaskari! Utupatie musaada juu ya waadui zetu, maana musaada wa mwanadamu haufai kitu. Mungu akikuwa upande wetu, tutashinda. Yeye ndiye atakayewaponda waadui zetu. Kwa mukubwa wa waimbaji. Wimbo wa Daudi. Usinyamaze, ee Mungu, ninayekusifu! Watu waovu na wadanganyifu wananishambulia, wanasema uongo juu yangu. Wanasema maovu juu yangu, na kunishambulia bila sababu. Ingawa niliwapenda, walinishitaki. Hata hivyo, niliwaombea. Wananilipa mabaya kwa mazuri yangu, na chuki kwa mapendo yangu. Umuweke mwamuzi mubaya juu ya adui yangu; na anayemushitaki amupeleke mbele ya baraza. Anapohukumiwa apatikane na kosa; malalamiko yake yahesabiwe kuwa kosa lingine. Siku za maisha yake zikuwe chache, mutu mwingine akamate kazi yake! Watoto wake wakuwe wayatima, na muke wake akuwe mujane! Watoto wake watangetange na kuombaomba; wafukuzwe katika mabaki ya nyumba zao! Anayemudai kitu amunyanganye mali yake yote, na wageni wakule mapato ya jasho lake! Kusikuwe mutu wa kumutendea mema, au kuwatunza watoto wake wayatima! Wazao wake wote wakufe; jina lake lisahauliwe katika kizazi kinachokuja! Yawe akumbuke uovu wa babu zake, zambi za mama yake zisifutwe hata kidogo! Yawe akumbuke zambi zao siku zote; lakini wao wenyewe wasahauliwe katika dunia. Mwovu huyo hajali kabisa kutenda mema, lakini anatesa wamasikini, wakosefu, na wenye moyo wenye kuvunjika mpaka kufa. Yeye alipenda kulaani watu; laana imupate yeye mwenyewe. Hakuwatakia wengine baraka; basi, asipate baraka yeye mwenyewe. Kwake kulaani ni kama kuvaa nguo; basi, laana hizo zimulowanishe kama maji, zimwingie katika mifupa yake kama mafuta. Laana zimufunike kama nguo, zimuzunguke siku zote kama mukaba. Yawe awalipe hayo hao watu wanaonishitaki, hao wanaosema mabaya juu yangu. Lakini, ee Yawe, Bwana wangu, unitendee kwa heshima ya jina lako. Wema wako ni muzuri. Basi, uniokoe! Mimi ni masikini na mukosefu; ninaumizwa mpaka ndani ya moyo wangu. Ninatoweka kama kivuli cha magaribi; nimepeperushwa kama nzige. Magoti yangu yanaregea kwa ajili ya kufunga kula chakula; nimebaki mifupa na ngozi. Watu wananichekelea; wanaponiona wanatikisa vichwa vyao kwa kunizarau. Unisaidie, ee Yawe, Mungu wangu; uniokoe kufuatana na wema wako. Uwaonyeshe watu kuwa wewe ndiwe uliyetenda hayo. Wewe, ee Yawe, ndiwe uliyefanya hivyo. Uwaache walaani, lakini wewe unibariki; wanaonishambulia wafezeheke, nami mutumishi wako nifurahi. Waadui zangu wazungukwe na mazarau; wajifunike haya yao kama vile nguo. Nitamushukuru sana Yawe kwa sauti; nitamusifu kati ya kundi kubwa la watu, kwa maana yeye anamutetea mukosefu, kwa kumwokoa kutoka kwa wale wanaomuhukumu kufa. Zaburi ya Daudi. Yawe anamwambia bwana wangu: “Ikaa na mamlaka kwa kuume kwangu mpaka nitakapowaweka waadui zako chini ya miguu yako.” Yawe ataeneza mamlaka yako kutoka Sayuni; utatawala juu ya waadui zako wote. Watu wako watajitolea, siku utakapokwenda kuwapiga waadui. Juu ya milima mitakatifu vijana wako watakufikia, kama umande unaotokeza asubui mapema. Yawe amekuapia hivi wala hatabadilisha nia yake: “Wewe ni kuhani milele kwa utaratibu wa ukuhani wa Melkisedeki.” Bwana wetu yuko karibu nawe; atawaponda wafalme atakapokasirika. Atayahukumu mataifa na kuwaua watu wengi; atawaponda waongozi kila nafasi katika dunia. Mufalme atakunywa maji ya kijito katika njia, kisha atainua kichwa kwa ushindi. Haleluia! Nitamushukuru Yawe kwa moyo wangu wote, katika mukutano wa watu wa usawa. Matendo ya Yawe ni makubwa sana! Wote wanaoyafurahia wanayachunguza. Kila anachofanya kimejaa utukufu na heshima; haki yake inadumu milele. Amesababisha matendo yake ya ajabu yakumbukwe; Yawe ni mwenye huruma na rehema. Anawapa chakula wenye kumwabudu; hasahau hata kidogo agano lake. Amewaonyesha watu wake nguvu ya matendo yake, amewapa inchi za mataifa mengine zikuwe mali yao. Matendo yake ni ya haki na ya kuaminika; kanuni zake zote ni za kutegemewa siku zote. Amri zake zinadumu milele; zimetolewa kwa uaminifu na usawa. Aliwakomboa watu wake na kufanya nao agano la milele. Yeye ni mutakatifu na wa kutisha sana! Kumwogopa Yawe ni musingi wa hekima; wote wanaotii amri zake wanajaliwa akili. Sifa zake zinadumu milele. Haleluia! Heri mutu anayemuheshimu Yawe, anayefurahia sana kushika amri zake. Wazao wake watakuwa wenye nguvu katika inchi; watoto wa watu wa usawa watapata baraka. Ndani ya nyumba yake kutakuwa mali nyingi; haki yake utadumu milele. Mutu wa usawa anaangaziwa mwangaza katika giza; yeye ni mwenye huruma, rehema, na haki. Mutu muzuri anakopesha bila faida; anafanya shuguli zake kwa kutumia haki. Hatashindwa hata kidogo; atakumbukwa milele. Haogopi habari mbaya; moyo wake unasimama imara na anamutegemea Yawe. Yuko imara ndani ya moyo, wala hataogopa; naye ataona waadui zake wakishindwa. Anatoa kwa moyo safi, anawapa wamasikini. Haki yake inadumu milele. Ana nguvu na sifa. Watu waovu wanaona hayo na kuuzika. Wanasaga meno kwa chuki na kutoweka. Matumaini ya mutu mubaya yanapotea bure. Haleluia! Enyi watumishi wa Yawe, musifu jina lake! Jina lake litukuzwe, sasa na hata milele. Kutoka mashariki na hata magaribi, litukuzwe jina la Yawe! Yawe anatawala juu ya mataifa yote, utukufu wake unafika juu ya mbingu. Nani anayekuwa kama Yawe, Mungu wetu? Yeye anakaa juu kabisa; lakini anachungulia chini, aangalie mbingu na dunia. Anamwinua muzaifu toka katika mavumbi, anamunyanyua mukosefu toka yalala, na kumuweka pamoja na wakubwa, pamoja na wakubwa wa watu wake. Anamurudishia heshima mwanamuke anayekuwa tasa; anamufurahisha kwa kumujalia watoto. Haleluia! Watu wa Israeli walipotoka Misri, wazao wa Yakobo walipotoka katika inchi ya kigeni, Yuda ikakuwa makao ya Mungu, Israeli ikakuwa urizi wake. Bahari iliona hayo ikakimbia; muto Yordani ukaacha kutiririka! Milima ilirukaruka kama kondoo dume; vilima vikaruka kama wana-kondoo! Ee bahari, nini iliyokufikia hata ukakimbia? Nawe Yordani, kwa nini uliacha kutiririka? Enyi milima, mbona muliruka kama kondoo dume? Nanyi vilima, namna gani mumeruka kama mwana-kondoo? Utetemeke, ee dunia, mbele ya Yawe; utetemeke mbele ya Mungu wa Yakobo, anayegeuza jiwe kubwa kuwa ziwa, nalo jiwe gumu kuwa chemichemi za maji! Si sisi, ee Yawe, si sisi; lakini wewe peke yako utukuzwe, kwa ajili ya wema na uaminifu wako. Kwa nini mataifa yanasema: “Mungu wenu yuko wapi?” Mungu wetu yuko mbinguni; yeye anafanya yote anayotaka. Miungu yao ni ya feza na zahabu; imetengenezwa kwa mikono ya wanadamu. Ina vinywa lakini haisemi. Ina macho lakini haioni. Ina masikio lakini haisikii. Ina pua lakini hainusi. Ina mikono lakini haipapasi. Ina miguu lakini haitembei. Haiwezi hata kidogo kutoa sauti. Wote wanaoitengeneza wanafanana nayo, na hata vilevile wote wanaoitumainia. Enyi Waisraeli, mumutumainie Yawe; yeye ndiye musaada wenu na ngao yenu. Enyi wazao wa Haruni, mumutumainie Yawe; yeye ndiye musaada wenu na ngao yenu. Enyi munaomwabudu Yawe, mumutumainie, yeye ndiye musaada wenu na ngao yenu. Yawe anatukumbuka na atatubariki. Atawabariki watu wa Israeli, atawabariki wazao wa Haruni, atawabariki wote wanaomwabudu, atawabariki wakubwa kama vile wadogo. Yawe awajalie muongezeke; awajalie muongezeke ninyi na wazao wenu! Mubarikiwe na Yawe, aliyeumba mbingu na dunia. Mbingu ni mali ya Yawe, lakini amewapa wanadamu dunia. Wafu hawamusifu Yawe, wala yeyote aliyeshuka katika kuzimu. Lakini ni sisi tutakaomusifu Yawe, tutamusifu sasa na hata milele. Haleluia! Ninamupenda Yawe, kwa maana ananisikia, maana amesikia kilio cha ombi langu. Yeye amenitegea sikio, hivyo nitamwomba muda wote wa maisha yangu. Hatari ya kifo ilinizunguka, vitisho vya kaburi vilinishika; nilisongwa na mahangaiko na huzuni. Kisha nikamulilia Yawe: “Ee Yawe, tafazali uniokoe!” Yawe ni mwenye huruma na haki; Mungu wetu ni mwenye rehema. Yawe anawalinda wajinga; nilipokuwa nimegandamizwa aliniokoa. Ukuwe na utulivu mukubwa, ee nafsi yangu, kwa vyote Yawe amenitendea. Ameniokoa toka kifo na kufuta machozi yangu; akanilinda nisianguke. Nitatembea mbele ya Yawe, katika inchi ya watu wenye kuwa wazima. Nilikuwa na imani hata niliposema: “Mimi nimetaabika sana.” Hata nilisema kwa hofu yangu: “Wanadamu wote hawawezi kutumainiwa!” Nitamurudishia Yawe nini, kwa vyote alivyonitendea? Nitamutolea sadaka ya divai kwa kumushukuru maana ameniokoa. Nitaomba kwa jina la Yawe. Nitamutimizia Yawe viapo vyangu, mbele ya watu wake wote. Kifo cha waaminifu wa Yawe si jambo dogo mbele yake. Ee Yawe, mimi ni mutumishi wako, mutumishi wako, mutoto wa mujakazi wako. Umenifungulia vifungo vyangu. Nitakutolea sadaka za shukrani. Nitaomba kwa jina la Yawe. Nitatimizia ahadi zangu kwa Yawe, mbele ya watu wake wote, katika kiwanja cha hekalu lake, katikati yako, ee Yerusalema. Haleluia! Enyi mataifa yote, mumusifu Yawe! Enyi watu wote, mumutukuze! Maana wema wake kwetu sisi ni mwingi; uaminifu wa Yawe unadumu milele! Haleluia! Mumushukuru Yawe, kwa sababu ni muzuri! Wema wake unadumu milele! Watu wa Israeli waseme: “Wema wake unadumu milele.” Wazao wa Haruni waseme: “Wema wake unadumu milele.” Wote wanaomwabudu Yawe waseme: “Wema wake unadumu milele.” Katika taabu yangu nilimwomba Yawe, naye akanisikia na kuniweka huru. Yawe yuko nami, siogopi kitu; mwanadamu ataweza kunifanya nini? Yawe yuko nami kwa kunisaidia; nami nitawaona waadui zangu wameshindwa. Afazali kumukimbilia Yawe kuliko kumutumainia mwanadamu. Afazali kumukimbilia Yawe, kuliko kuwatumainia waongozi wa dunia. Mataifa yote yalinizunguka, lakini kwa jina la Yawe nikayaangamiza! Yalinizunguka kila upande, lakini kwa jina la Yawe, nikayaangamiza! Yalinizunguka, mengi kama nyuki, lakini yakateketea kama kichaka ndani ya moto; kwa jina la Yawe niliyaangamiza! Nilishambuliwa sana karibu nishindwe, lakini Yawe alinisaidia. Yawe ni nguvu yangu kubwa; yeye mwenyewe ndiye wokovu wangu. Sauti za furaha ya ushindi zikasikilika katika hema za watu wa haki: “Mukono wa Yawe umetenda mambo makubwa! Mukono wa nguvu wa Yawe umeleta ushindi! Mukono wa Yawe umetenda mambo makubwa!” Sitakufa. Nitaishi na kueleza matendo ya Yawe. Yawe ameniazibu sana, lakini hakuniachilia nikufe. Munifungulie milango ya watu wa haki, niingie na kumushukuru Yawe! Huu ndio mulango wa Yawe, watu wa haki watapitia humo. Ninakushukuru, ee Yawe, kwa kunijibu; kwa sababu wewe ni wokovu wangu. Jiwe lililokataliwa na wajengaji, limekuwa sasa jiwe kubwa la musingi. Ni Yawe aliyefanya jambo hili, nalo ni ajabu sana kwetu. Hii ndiyo siku aliyoifanya Yawe; tushangilie na kufurahi. Tafazali utuokoe, ee Yawe! Tafazali utubariki, ee Yawe! Abarikiwe huyu anayekuja kwa jina la Yawe! Tunawabariki kutoka katika nyumba ya Yawe. Yawe ni Mungu; yeye ametujalia mwangaza wake. Mushike matawi katika mikono, mukiandamana mpaka kwenye mazabahu. Wewe ni Mungu wangu, ninakushukuru; ninakutukuza, ee Mungu wangu. Mumushukuru Yawe kwa sababu ni muzuri, kwa maana wema wake unadumu milele. Heri watu wanaoishi katika ukamilifu, wanaofuata sheria ya Yawe. Heri wanaoshika maagizo yake, wanaomutafuta kwa moyo wao wote, watu wasiotenda uovu hata kidogo, lakini wanafuata siku zote njia zake. Ee Mungu, umetupatia kanuni zako kusudi tuzishike kwa uangalifu. Heri mwenendo wangu ungeimarika kwa kuyafuata masharti yako! Nikichunguza amri zako zote, hapo kweli sitapata haya. Nitakusifu kwa moyo wenye kunyooka, nikijifunza maamuzi yako ya haki. Nitafuata masharti yako; usiniache hata kidogo. Namna gani kijana ataweza kujichunga katika njia safi? Ni kwa kufuatilia neno lako. Ninakutafuta kwa moyo wote; usiniachilie kugeuka mbali na amri zako. Nimeshika neno lako ndani ya moyo wangu, kusudi nisikukosee. Utukuzwe, ee Yawe! Unifundishe masharti yako. Nitarudiliarudilia kwa sauti maamuzi yako yote uliyotoa. Ninafurahi kufuata maagizo yako, kuliko kuwa na utajiri mwingi. Ninafikiri juu ya kanuni zako, na kuangalia njia zako. Ninafurahia masharti yako; sitasahau neno lako. Unitendee mimi mutumishi wako kwa wema, nipate kuishi na kushika neno lako. Uyafungue macho yangu, nipate kuona maajabu ya sheria yako. Mimi ni mugeni tu hapa katika dunia; usinifiche amri zako. Roho yangu inaugua kwa hamu kubwa ya kutaka kujua siku zote maamuzi yako. Wewe unawakaripia wenye kiburi waliolaaniwa, ambao wanageuka mbali na amri zako. Uniepushe na matusi na mazarau yao, maana ninafuata maagizo yako. Hata kama wakubwa wananifanyia shauri baya, mimi mutumishi wako nitafikiri juu ya masharti yako. Maagizo yako ndiyo furaha yangu; hayo ndio washauri wangu. Ninagaagaa chini ndani ya mavumbi; unirudishie uzima sawa ulivyoahidi. Nimeungama niliyotenda, nawe ukanijibu; unifundishe masharti yako. Unifundishe namna ya kushika kanuni zako, nami nitafikiri juu ya matendo yako ya ajabu. Ninalia kwa uchungu; unirudishie nguvu kama ulivyoahidi. Uniepushe na njia za upotovu; unifundishe kwa huruma sheria yako. Nimechagua njia ya uaminifu; nitafuatilia maamuzi yako. Ninashikamana na maagizo yako, ee Yawe; usikubali nipatishwe haya! Nitafuatilia amri zako, maana unanifungua akili zaidi. Ee Yawe, unifundishe kutii masharti yako, nami nitayashika mpaka mwisho. Unieleweshe nipate kushika sheria yako, niifuate kwa moyo wangu wote. Uniongoze katika njia ya amri zako, maana humo ninapata furaha yangu. Uvute moyo wangu kufuata maagizo yako, na si kwa ajili ya kupata faida isiyofaa. Uniepushe nisifuate mambo ya ovyo; unionyeshe njia yako, unipe uzima. Unitimizie mimi mutumishi wako ahadi yako; ahadi unayowapa wale wanaokuheshimu. Uniepushe na matusi ninayoogopa; maana maamuzi yako ni mema. Ninatamani sana kutii kanuni zako; unirudishie uzima maana wewe ni wa haki. Wema wako unifikie, ee Yawe; uniokoe kama ulivyoahidi. Hapo nitaweza kuwajibu hao wanaonitukana, maana mimi ninatumainia neno lako. Unijalie kusema ukweli wako siku zote, maana ninatumainia maamuzi yako. Nitatii sheria yako siku zote, nitaishika milele na milele. Nitaishi katika uhuru kamili, maana ninashugulika na kanuni zako. Nitawatangazia wafalme maagizo yako, wala sitaona haya. Furaha yangu ni kuzitii amri zako, ambazo mimi ninazipenda. Ninaziheshimu na kuzipenda amri zako; nitafikiri juu ya masharti yako. Ukumbuke ahadi yako kwangu mimi mutumishi wako, ahadi ambayo imenipa matumaini. Hata katika taabu, inanituliza, maana ahadi yako inanipa uzima. Wasiomujali Mungu wananizarau siku zote, lakini mimi sigeuki mbali na sheria yako. Ninapokumbuka maamuzi yako ya tangu zamani, ninafarijika, ee Yawe. Ninashikwa na hasira kali, ninapoona waovu wakivunja sheria yako. Masharti yako yamekuwa wimbo wangu, nikikuwa huku kama mugeni. Usiku ninakukumbuka, ee Yawe, na kushika sheria yako. Hili ni pato langu, kwamba ninashika kanuni zako. Wewe, ee Yawe, ndiwe hitaji langu lote; ninaahidi kushika maneno yako. Ninataka kukupendeza kwa moyo wangu wote; unionee huruma kama ulivyoahidi! Nimefikiri juu ya mwenendo wangu, na nimerudi nifuate maagizo yako. Bila kukawia ninafanya haraka kushika amri zako. Waovu wametega mitego waninase, lakini mimi sisahau sheria yako. Usiku kati ninaamuka kwa kukusifu, kwa sababu ya maamuzi yako ya haki. Mimi ni rafiki ya wote wanaokuheshimu, rafiki ya wanaoshika kanuni zako. Dunia imejaa wema wako, ee Yawe, unifundishe masharti yako. Umenitendea vizuri mimi mutumishi wako, kama ulivyoahidi, ee Yawe. Unipe hekima na ufahamu, maana ninaaminia amri zako. Mbele sijateswa nilikuwa nimepotea, lakini sasa ninashika neno lako. Wewe ni muzuri na unatenda mazuri; unifundishe masharti yako. Wenye kiburi wanasema uongo juu yangu, lakini mimi ninashika kanuni zako kwa moyo wote. Mioyo yao inafungana sana, lakini mimi ninafurahia sheria yako. Nimefaidika kutokana na taabu yangu, maana imeniwezesha kujifunza masharti yako. Sheria uliyoweka ni bora kwangu, kuliko mali zote za dunia. Kwa mikono yako wewe mwenyewe uliniumba; unijalie akili nijifunze amri zako. Wanaokuheshimu wataniona na kufurahi, maana tumaini langu liko katika neno lako. Ninajua kwamba maamuzi yako ni ya haki, ee Yawe, na kwamba umeniazibu maana wewe ni mwaminifu. Wema wako unifariji, kama ulivyoniahidi mimi mutumishi wako. Unionee rehema nipate kuishi, maana sheria yako ni furaha yangu. Wenye kiburi wafezeheke, maana wananisumbua na maneno ya uongo, lakini mimi nitafikiri juu ya kanuni zako. Wote wanaokuheshimu wakuje kwangu, wapate kujua maagizo yako. Moyo wangu ukuwe mukamilifu juu ya masharti yako, kusudi nisifezeheke. Ninachoka kwa kukungojea uniokoe; ninatumainia neno lako. Macho yangu yanafifia nikingojea ulichoahidi. Ninauliza: “Utakuja wakati gani kunifariji?” Nimekunjamana kama mufuko wa ngozi katika moshi, hata hivyo sijasahau masharti yako. Mimi mutumishi wako nitavumilia mpaka wakati gani? Utawaazibu wakati gani wale wanaonitesa? Wenye kiburi wamenichimbia mashimo, watu ambao hawafuati sheria yako. Amri zako zote ni za kuaminiwa; watu wananitesa bila haki; unisaidie! Walifikia karibu ya kuniangamiza, lakini mimi sikuvunja kanuni zako. Kwa wema wako, unirudishie uzima, nipate kufuata maagizo uliyotangaza. Neno lako, ee Yawe, linadumu milele; linasimama imara mbinguni. Uaminifu wako unadumu kwa vizazi vyote, umeweka dunia pahali pake, nayo inadumu. Kwa amri yako viumbe vyote viko leo, maana vitu vyote ni chini ya mamlaka yako. Kama sheria yako isingekuwa furaha yangu, ningalikwisha kuangamia kwa taabu zangu. Sitasahau hata kidogo kanuni zako, maana kwa njia yao unanirudishia uzima. Mimi ni wako, uniokoe, maana nimejitoa kushika kanuni zako. Waovu wananivizia wapate kuniua; lakini mimi ninafikiri juu ya maagizo yako. Nimetambua kwamba kila kitu kina mwisho, lakini amri yako haina mupaka. Ninapenda sana sheria yako! Ninafikiri juu yake muchana kutwa! Amri yako iko nami siku zote, inanipa hekima kuliko waadui zangu. Ninaelewa kuliko walimu wangu wote, kwa sababu ninafikiri juu ya maagizo yako. Ninawapita wazee kwa akili yangu, kwa sababu ninashika kanuni zako. Ninajizuiza kufuata njia mbaya, kusudi nipate kushika neno lako. Sikugeuka mbali na maamuzi yako, maana wewe mwenyewe ulinifundisha. Maagizo yako ni matamu sana kwangu; ni matamu kuliko asali! Kwa kanuni zako ninapata hekima, kwa hiyo ninachukia kila mwenendo mubaya. Neno lako ni taa ya kuniongoza, na mwangaza katika njia yangu. Nimeapa na kuhakikisha kiapo changu, kwamba nitashika maamuzi yako ya haki. Ee Yawe, ninateseka sana; unirudishie uzima kama ulivyoahidi. Ee Yawe, upokee maombi yangu ya shukrani, na kunielezea maamuzi yako. Maisha yangu yako katika hatari siku zote, lakini sisahau sheria yako. Waovu wamenitegea mitego, lakini sigeuki mbali na kanuni zako. Maagizo yako ni urizi mukubwa kwangu milele; hayo ni furaha ya moyo wangu. Nimekusudia kwa moyo wote kufuata masharti yako milele. Ninachukia watu wanafiki, lakini ninapenda sheria yako. Wewe ni ngao yangu, na kimbilio langu; ninaweka tumaini langu katika neno lako. Muondoke kwangu, enyi waovu, kusudi nipate kushika amri za Mungu wangu. Uniimarishe sawa ulivyoahidi, nami nitaishi; usikubali nifezeheke katika tumaini langu. Unishike nipate kuwa salama, nikuwe siku zote musikilivu kwa masharti yako. Unawakataa wote wanaogeuka mbali na masharti yako; mawazo yao maovu ni ya bure. Unaona waovu wote kama vile takataka, kwa hiyo mimi ninapenda maagizo yako. Ninatetemeka kwa kukuogopa wewe; nimejaa hofu kwa sababu ya maamuzi yako. Nimefanya mambo mema na ya haki; usiniache katika makucha ya waadui zangu. Uhakikishe kunisaidia mimi mutumishi wako; usikubali wenye kiburi wanitese. Macho yangu yanafifia nikingojea uniokoe, nikingojea utimize uliyoahidi. Unitendee mimi mutumishi wako kadiri ya wema wako, unifundishe masharti yako. Mimi ni mutumishi wako. Unipe akili nipate kujua maagizo yako. Ee Yawe, sasa ni wakati wa kutenda kitu, kwa maana watu wanavunja sheria yako. Kweli, ninapenda amri zako, kuliko hata zahabu safi kabisa. Kwa hiyo, ninafuata kanuni zako zote; ninachukia kila njia ya upotovu. Maagizo yako ni ya ajabu; kwa hiyo ninayashika kwa moyo wote. Maelezo ya mafundisho yako yanaleta mwangaza; yanawapa akili wajinga. Ninafungua kinywa kwa hamu kubwa, maana ninatamani sana amri zako. Unigeukie na kunionea huruma, kama unavyowatendea wanaokupenda. Uniimarishie hatua zangu kama ulivyoahidi; usikubali mimi nitawaliwe na uovu. Unikomboe kutoka mateso ya wanadamu, kusudi nipate kushika kanuni zako. Uniangazie uso wako kwa wema, unifundishe masharti yako. Macho yangu yanatiririka machozi kama muto, kwa sababu watu hawaishiki sheria yako. Ee Yawe, wewe ni wa haki; na hukumu zako ni za usawa. Umetoa maagizo yako, kwa haki na uaminifu. Upendo wangu kwako unanifanya niwake hasira, maana waadui zangu hawajali maneno yako. Ahadi yako ni hakika kabisa, nami mutumishi wako ninaipenda. Mimi ni mudogo na ninazarauliwa; hata hivyo sisahau kanuni zako. Haki yako ni haki ya milele; sheria yako ni ya kweli. Taabu na huzuni vimenipata, lakini amri zako ndizo furaha yangu. Maagizo yako ni ya haki siku zote; unijalie akili nipate kuishi. Ninakulilia kwa moyo wangu wote; unijibu, ee Yawe, nifuate masharti yako. Ninakulilia, uniokoe nipate kushika maagizo yako. Ninaamuka mbele ya mapambazuko na kukuomba musaada; ninaweka tumaini langu katika maneno yako. Ninakaa macho wazi usiku kucha, kusudi nifikiri juu ya ahadi zako. Kwa wema wako, ee Yawe, unisikilize; kwa haki yako, unirudishie uzima. Wale wanaonitesa vibaya wanakaribia, hao wako mbali kabisa na sheria yako. Lakini wewe ni karibu nami, ee Yawe, na amri zako zote ni za kuaminiwa. Tangu zamani, nimejifunza maagizo yako ambazo umeziweka hata zidumu milele. Uangalie mateso yangu, uniokoe, kwa maana sikusahau sheria yako. Unitetee na kunikomboa; unirudishie uzima kama ulivyoahidi. Waovu hawataokolewa hata kidogo, maana hawajali juu ya masharti yako. Rehema yako ni kubwa, ee Yawe, unirudishie uzima kama ulivyoahidi. Waadui na watesaji wangu ni wengi, lakini mimi sigeuki mbali na maagizo yako. Ninapowaona waasi hao ninachukizwa sana, kwa sababu hawashiki amri zako. Angalia, ee Mungu, ninavyopenda kanuni zako! Unirudishie uzima kadiri ya wema wako. Kifungo cha neno lako ni ukweli, maamuzi yako yote ya haki yanadumu milele. Wakubwa wananitesa bila sababu, lakini mimi ninaheshimu maneno yako kwa moyo wote. Ninafurahi kwa sababu ya neno lako, kama mutu aliyekuta kitu cha bei kali. Ninachukia kabisa uongo, lakini ninapenda sheria yako. Ninakusifu mara saba kila siku, kwa sababu ya maamuzi yako ya haki. Wanaopenda sheria yako wana amani kubwa; hakuna kinachoweza kuwaangusha. Ee Yawe, ninakungojea uniokoe; mimi ninatimiza amri zako. Ninashika maagizo yako; ninayapenda kwa moyo wote. Ninashika kanuni na maagizo zako; wewe unaona mwenendo wangu wote. Kilio changu kikufikie, ee Yawe! Unijalie akili kama ulivyoahidi. Ombi langu likufikie; uniokoe kama ulivyoahidi. Midomo yangu itatangaza sifa zako, maana unanifundisha masharti yako. Nitaimba juu ya neno lako, maana amri zako zote ni za haki. Ukuwe siku zote tayari kunisaidia, maana nimeamua kufuata kanuni zako. Ninatamani sana uniokoe, ee Yawe; sheria yako ndiyo furaha yangu. Unijalie kuishi nipate kukusifu; na maamuzi yako yanisaidie. Ninatangatanga kama kondoo aliyepotea; ukuje kunitafuta mimi mutumishi wako, maana sikusahau amri zako. Wimbo wa safari za kidini. Katika taabu yangu nilimwita Yawe, naye akanijibu. Uniokoe, ee Yawe, kutoka watu wadanganyifu na waongo. Enyi watu wadanganyifu, mutapewa kitu gani? Mutaazibiwa namna gani? Kwa mishale mikali ya waaskari, kwa makaa ya moto mukali! Ole wangu maana ninaishi kama mugeni huko Meseki; ninaishi kama mugeni katika mahema ya Kedari. Nimeishi muda murefu sana kati ya watu wanaochukia amani! Ninaposema kwamba ninataka amani, wao wanataka tu vita. Wimbo wa safari za kidini. Ninainua macho kwenye milima. Musaada wangu unatoka wapi? Musaada wangu unatoka kwa Yawe, aliyeumba mbingu na dunia. Hatakuacha uanguke; mulinzi wako hasinzii. Kweli mulinzi wa Israeli hasinzii wala halali. Yawe ni mulinzi wako; yuko upande wako wa kuume kwa kukukinga. Muchana jua halitakuchoma, wala mwezi hautakuzuru usiku. Yawe atakukinga na uovu wote; atayalinda salama maisha yako. Yawe atakulinda katika shuguli zako zote tangu sasa na hata milele. Wimbo wa Safari za kidini. Wa Daudi. Nilifurahi waliponiambia: “Twende kwenye nyumba ya Yawe.” Sasa tuko tumesimama kwenye milango yako, ee Yerusalema! Yerusalema ni muji uliojengwa kusudi makundi ya watu yakutane humo. Humo ndimo makabila yanamofika, ndiyo, makabila ya Yawe, kwa kumushukuru Yawe kama Waisraeli walivyoagiza. Humo kulikuwa viti vya kifalme kwa kuamua maneno, ndivyo viti vya ukoo wa Daudi. Muuombee Yerusalema amani mukisema: “Wote wanaokupenda wakae katika amani! Ndani ya kuta zinazokuzunguka kuwe amani, nao usalama ukuwe ndani ya nyumba zako nzuri!” Kwa ajili ya jamaa na wandugu zangu, ee Yerusalema, ninakutakia amani! Kwa ajili ya nyumba ya Yawe, Mungu wetu, ninakuombea upate uheri! Wimbo wa safari za kidini. Ninainua macho kwako, ee Yawe, wewe unayeikaa huko juu mbinguni! Kama watumishi wanavyomutegemea bwana wao, kama mujakazi anavyomutegemea bibi mukubwa wake, ndivyo nasi tunavyokutegemea wewe, ee Yawe, Mungu wetu, mpaka hapo utakapotuonea huruma. Utuhurumie, ee Yawe, utuhurumie, maana tumezarauliwa kupita kipimo. Tumeshiba muda murefu mazarau ya watajiri, nayo masimango ya wenye kiburi. Wimbo wa safari za kidini. Ninyi wote munaokuwa katika Israeli museme: “Kama Yawe asingalikuwa upande wetu”. “Kama Yawe asingalikuwa upande wetu, wakati ule tuliposhambuliwa na waadui, hakika tungalimezwa tukikuwa wazima, wakati hasira yao ilipowaka juu yetu. Tungalichukuliwa na maji mengi, tungalifunikwa na muto. Tungalizamishwa na maporomoko ya maji!” Yawe atukuzwe! Hakutuachilia katika meno yao. Tumeponyoka kama ndege katika mutego; mutego umefyatuka, nasi tukaponyoka. Musaada wetu unatoka kwa Yawe, aliyeumba mbingu na dunia. Wimbo wa safari za kidini. Wanaomutegemea Yawe, wako kama mulima Sayuni, ambao hautikisiki lakini unabaki imara siku zote. Kama vile milima inavyozunguka Yerusalema, ndivyo Yawe anavyozunguka watu wake, tangu sasa na hata milele. Waovu hawataendelea kutawala inchi ya watu wa haki, kusudi watu wa haki nao wasifanye maovu. Ee Yawe, ukuwe mwema kwa watu wema, kwa wale wenye moyo wenye kunyooka. Lakini wanaogeuka na kufuata njia zao mbaya, uwatoweshe pamoja na watenda maovu. Amani ikuwe na Israeli! Wimbo wa safari za kidini. Yawe alipoturudisha tena Sayuni, tulikuwa kama watu wanaoota ndoto! Hapo kinywa chetu kilijaa kicheko; tulishangilia kwa furaha. Nao watu wa mataifa mengine walisema: “Yawe amewatendea mambo makubwa!” Kweli Yawe alitutendea maajabu, tulifurahi kweli kweli! Ee Yawe, utengeneze hali yetu, kama vile maji yanavyorudi katika jangwa la Negebu. Wanaopanda kwa machozi, watavuna kwa shangwe. Wanaokwenda kupanda mbegu wakilia, watarudi kwa furaha wakichukua mavuno. Wimbo wa safari za kidini: wa Solomono. Yawe asipoijenga nyumba, wanaoijenga wanajisumbua bure. Yawe asipoulinda muji, wanaoulinda wanakesha bure. Munajisumbua bure kuamuka asubui mapema na kuchelewa kwenda kupumzika magaribi, mujipatie chakula kwa jasho lenu. Mungu anatimiza mahitaji ya wapendwa wake hata wanapolala. Watoto ni urizi kutoka kwa Yawe; uzao ni zawadi yake kwetu sisi. Watoto wanaokuwa na nguvu, ni kama mishale katika mikono ya askari. Heri mutu anayekuwa na mishale hiyo kwa wingi. Hatashindwa atakaposamba na waadui zake kwenye tribinali. Wimbo wa safari za kidini. Heri wote wanaomwabudu Yawe, wanaoishi kufuatana na amri zake. Utapata matunda ya jasho lako, utafurahi na kupata uheri. Muke wako atakuwa kama muzabibu wenye matunda mengi; watoto wako kama vichipukizi vya muzeituni kuzunguka meza yako. Kweli, hivi ndivyo atakavyobarikiwa mutu anayemwabudu Yawe. Yawe akubariki kutokea Sayuni! Uone uheri wa Yerusalema, siku zote za maisha yako. Uishi na hata uwaone wajukuu wako! Amani ikuwe na Israeli! Wimbo wa safari za kidini. Kila mutu katika Israeli aseme: “Nimesumbuliwa vibaya tangu ujana wangu”. Nimesumbuliwa vibaya tangu ujana wangu, lakini hawakunishinda. Walinikata vidonda katika mugongo, kama wanavyolima matuta katika shamba. Lakini Yawe ni mwenye haki; ametutosha katika utumwa wa hao waovu. Wafezeheke na kurudishwa nyuma, wote wale wanaouchukia Sayuni. Wakuwe kama nyasi juu ya paa la nyumba, ambazo zinanyauka mbele ya kukomaa, anayezikata hajazi kitanga cha mukono, wala anayezikusanya haenezi fungu. Naye anayepita karibu asiwaambie: “Yawe awabariki! Tunawabariki kwa jina la Yawe!” Wimbo wa safari za kidini. Tokea humu katika taabu inayonilemea, ninakulilia, ee Yawe. Ee Bwana, usikie sauti yangu, ulitegee ombi langu sikio. Ee Yawe, kama ungekumbuka maovu yetu, nani, ee Bwana wetu, angeweza kuishi? Lakini kwako tunapata usamehe, kusudi sisi tukuheshimu. Ninamutumainia Yawe kwa moyo wangu wote. Ninaaminia sana neno lake. Ninamungojea Yawe kuliko vile wazamu wanavyongojea mapambazuko, ndiyo, kuliko vile wazamu wanavyongojea mapambazuko. Ee Israeli, umutumainie Yawe, maana Yawe ni mwenye wema, naye ana nguvu kubwa ya kutukomboa. Yeye atawakomboa watu wa Israeli kutoka katika maovu yao yote. Wimbo wa safari za kidini: wa Daudi. Ee Yawe, sina moyo wa majivuno; wala macho yangu si ya kiburi. Sijishugulishi na mambo makubwa, yale yanayokuwa ya ajabu sana kwangu. Lakini nafsi yangu imetulia na kuwa na amani, kama mutoto muchanga anavyotulia na mama yake; ndivyo nafsi yangu inavyokuwa na utulivu. Ee Israeli, umutumainie Yawe, tangu sasa na hata milele. Wimbo wa safari za kidini. Ee Yawe, umukumbuke Daudi, kumbuka taabu zote alizopata. Ukumbuke ahadi aliyokupa, ee Yawe, ndicho kiapo alichokuapia, ewe Mwenye Nguvu wa Yakobo. Alisema: “Sitaingia ndani ya nyumba yangu, wala kulala ndani ya kitanda changu, sitakubali kulala usingizi, wala kusinzia, mpaka nikutayarishie wewe Yawe nafasi ya kukaa, ndiyo makao yako, ewe Mwenye Nguvu wa Yakobo!” Tulisikia wakisema: “Sanduku la Agano ni kule Efurata, tulilikuta katika mashamba ya Yearimu.” Basi! Tuende kwa nyumba ya Mungu, tuabudu mbele ya kiti chake cha kifalme! Simama sasa, ee Yawe, ukuje kwenye pumziko lako, pamoja na Sanduku la Agano la uwezo wako! Makuhani wako wakuwe watu wa haki siku zote; na waaminifu wako wapige vigelegele vya furaha! Kwa ajili ya Daudi, mutumishi wako, usimukatae huyo mufalme uliyemuchagua. Yawe alimwapia Daudi kiapo cha hakika, kiapo hiki ambacho hatakivunja: “Nitamuweka mumoja wa wazao wako mwenyewe, kuwa mufalme nyuma yako. Watoto wako wakishika agano langu, na kufuata maagizo nitakayowapa, watoto wao pia watakuwa wafalme kama wewe milele.” Yawe ameuchagua Sayuni, ametaka ukuwe makao yake. Yeye anasema: “Hapa ndipo nitakapokaa milele, ndipo makao yangu, maana nimepachagua. Nitaubariki Sayuni kwa mahitaji yake; nitawashibisha chakula wamasikini wake. Nitawavalisha makuhani wake katika wokovu, waaminifu wake watapiga vigelegele vya furaha. Humo nitamuchipukiza mufalme shujaa wa ukoo wa Daudi. Kama vile taa inayowaka, nitamwimarisha mufalme niliyemuchagua. Waadui zake nitawavalisha haya; lakini yeye nitamuvalisha utukufu wa kifalme.” Wimbo wa safari za kidini: wa Daudi. Ni jambo zuri na la kupendeza sana kwa ndugu kuishi pamoja kwa umoja. Ni kama mafuta mazuri yanayotiririka juu ya kichwa, mpaka kwenye ndevu za Haruni, mpaka juu ya upindo wa nguo yake kwenye shingo. Ni kama umande wa mulima Hermoni, unaoanguka juu ya vilima vya Sayuni! Kutoka huko Yawe anatoa baraka, ndio uzima wa milele. Wimbo wa safari za kidini. Mukuje kumusifu Yawe, enyi watumishi wake wote, enyi wote munaotumikia ndani ya nyumba yake usiku. Muinue mikono kuelekea pahali patakatifu, na kumutukuza Yawe! Yawe akubariki kutoka Sayuni; yeye aliyeumba mbingu na dunia. Haleluia! Musifu jina la Yawe, mumusifu, enyi watumishi wake. Mumusifu, enyi munaokaa katika nyumba yake, ndani ya viwanja vya nyumba ya Mungu wetu! Mumusifu Yawe kwa sababu yeye ni muzuri; mumutukuze kwa nyimbo, maana inafaa. Yawe amemuchagua Yakobo kuwa wake, watu wa Israeli kuwa mali yake mwenyewe. Ninajua hakika kwamba Yawe ni mukubwa; Bwana wetu ni mukubwa kupita miungu yote. Yawe anafanya chochote anachotaka, mbinguni, katika dunia, ndani ya bahari na shimo ndefu. Analeta mawingu kutoka miisho ya dunia, anapiga umeme na kunyesha mvua, anavumisha upepo kutoka gala zake. Aliwaua wazaliwa wa kwanza huko Misri, wazaliwa wa watu na wa nyama vilevile. Alifanya miujiza na maajabu kwako, ee Misri, mufalme wa Misri na wakubwa wake wote. Aliangamiza mataifa mengi, akawaua wafalme wenye nguvu kama vile Sihoni mufalme wa Waamori, Ogi mufalme wa Basani, na wafalme wote wa Kanana. Alikamata inchi zao kuwa urizi wa watu wake; zikuwe urizi wa watu wake Israeli. Jina lako, ee Yawe, linadumu milele, utakumbukwa nyakati zote. Yawe atawatetea watu wake; na kuwaonea huruma watumishi wake. Miungu ya uongo ya mataifa ni feza na zahabu, imetengenezwa kwa mikono ya wanadamu. Ina vinywa, lakini haisemi; ina macho, lakini haioni. Ina masikio, lakini haisikii; wala haiwezi hata kuvuta pumzi. Wote walioifanya wafanane nayo, kila mumoja anayeitegemea! Enyi watu wa Israeli, mumutukuze Yawe! Enyi makuhani, mumutukuze Yawe! Enyi Walawi, mumutukuze Yawe! Enyi munaomwabudu Yawe, mumutukuze! Atukuzwe Yawe katika Sayuni, atukuzwe katika makao yake Yerusalema. Haleluia! Mumushukuru Yawe kwa sababu yeye ni muzuri! Wema wake unadumu milele! Mumushukuru Mungu wa miungu. Wema wake unadumu milele. Mumushukuru Bwana wa wabwana. Wema wake unadumu milele. Yeye peke yake anatenda miujiza mikubwa. Wema wake unadumu milele. Aliumba mbingu kwa hekima. Wema wake unadumu milele. Alitengeneza inchi juu ya vilindi vya maji. Wema wake unadumu milele. Aliumba jua, mwezi na nyota. Wema wake unadumu milele. Aliumba jua litawale muchana. Wema wake unadumu milele. Aliumba mwezi na nyota vitawale usiku. Wema wake unadumu milele. Aliwaua wazaliwa wa kwanza wa Misri. Wema wake unadumu milele. Akawaondoa watu wa Israeli kutoka huko. Wema wake unadumu milele. Akawaondoa kwa mukono wake wenye nguvu na mamlaka. Wema wake unadumu milele. Aligawanya bahari Nyekundu katika sehemu mbili. Wema wake unadumu milele. Akawapitisha watu wa Israeli humo. Wema wake unadumu milele. Lakini akazamisha mufalme wa Misri na waaskari wake humo. Wema wake unadumu milele. Aliongoza watu wake katika jangwa. Wema wake unadumu milele. Alipiga wafalme wenye nguvu. Wema wake unadumu milele. Akaua wafalme wenye utukufu. Wema wake unadumu milele. Akamwua Sihoni, mufalme wa Waamori. Wema wake unadumu milele. Akamwua Ogi, mufalme wa Basani. Wema wake unadumu milele. Akakamata inchi zao kuwa urizi wa watu wake. Wema wake unadumu milele. Ni urizi wa Israeli, mutumishi wake. Wema wake unadumu milele. Alitukumbuka wakati wa uzaifu wetu. Wema wake unadumu milele. Akatuokoa kutoka waadui zetu. Wema wake unadumu milele. Anapatia kila kiumbe chenye uzima chakula. Wema wake unadumu milele. Mumushukuru Mungu wa mbinguni. Wema wake unadumu milele! kandokando ya mito ya Babeli tuliikaa tukilia, tulipokumbuka Sayuni. Katika miti ya inchi ile, tulitundika zeze zetu. Waliotupeleka kuwa watumwa walitaka tuwaimbie; watesaji wetu walitaka tuwafurahishe, wakituambia: “Mutuimbie nyimbo zimoja za Sayuni!” Namna gani tunaweza kuimba wimbo wa Yawe katika inchi ya kigeni? Ee Yerusalema, kama nikikusahau, mukono wangu wa kuume ukauke! Ulimi wangu ukuwe muzito, kama nisipokukumbuka wewe, ee Yerusalema, nisipokufurahia kuliko furaha yangu kubwa! Ee Yawe, usisahau mambo Waedomu waliyotenda, siku ile Yerusalema iliponyanganywa; kumbuka maneno haya waliyosema: “Mubomoe Yerusalema! Muongoe hata na misingi yake!” Ee Babeli, muharibifu wee! Heri yule atakayekulipiza mabaya uliyotutendea! Heri yule atakayetwaa watoto wako na kuwapondaponda juu ya jiwe! Zaburi ya Daudi. Ninakushukuru, ee Yawe, kwa moyo wangu wote, ninaimba sifa zako mbele ya miungu. Ninainama uso mpaka chini kuelekea hekalu lako takatifu. Ninalisifu jina lako, kwa sababu ya wema na uaminifu wako. Umeheshimisha jina lako na neno lako kuliko vitu vyote. Nilipokulilia, wewe ulinijibu; umeniongezea nguvu yangu. Wafalme wote katika dunia watakusifu, ee Yawe, kwa sababu wameyasikia maneno yako. Wataimba sifa za matendo yako, ee Yawe, kwa maana utukufu wako ni mukubwa. Ee Yawe, ingawa wewe uko juu ya wote, unawaangalia wanyenyekevu kwa wema; lakini, unatambua wenye kiburi kwa mbali. Hata nikisongwa na taabu, wewe unanilinda. Unanyoosha mukono wako juu ya waadui zangu wakali, kwa nguvu yako kubwa unaniokoa. Ee Yawe, utatimiza yote uliyoniahidia. Wema wako, ee Yawe, unadumu milele. Usisahau kazi ya mukono wako mwenyewe. Kwa mukubwa wa waimbaji. Zaburi ya Daudi. Ee Yawe, wewe umenichunguza, wewe unanijua mpaka ndani. Nikiikaa au nikisimama, wewe unajua; wewe unajua kila kitu ninachofikiri juu yake. Nikienda au nikipumzika, unatambua; wewe unajua shuguli zangu zote. Mbele sijasema neno lolote, wewe, ee Yawe, unalijua kabisa. Uko kila upande wangu, mbele na nyuma; unaniwekea mukono wako kwa kunilinda. Ufahamu wako unapita akili yangu; ni mukubwa sana, siwezi kuuelewa. Nikimbilie wapi ambako roho yako haiko? Niende wapi ambako wewe hauko? Nikipanda juu mbinguni, wewe ni kule; nikijilaza chini katika kuzimu, wewe ni kule. Nikiruka mpaka mbali sana upande wa mashariki, au hata kwa miisho upande wa magaribi, wewe uko hata kule kwa kuniongoza; mukono wako wa kuume utanilinda. Kama ningeliomba giza linifunike, giza linizunguke pahali pa mwangaza, kwako giza si giza hata kidogo, na usiku unaangaa kama muchana; kwako giza na mwangaza ni sawa. Wewe uliniumba mwili wangu wote; ulinitengeneza katika tumbo la mama yangu. Ninakusifu maana umeniumba kwa namna ya ajabu. Matendo yako ni ya ajabu. Wewe unanijua kabisa kabisa. Umbo langu halikufichikwa kwako nilipoumbwa kwa uficho, nilipotengenezwa ndani ya tumbo la mama yangu. Wewe uliniona hata mbele sijazaliwa. Uliandika kila kitu katika kitabu chako; siku zangu zote ulizipanga, hata mbele hakujakuwa ile ya kwanza. Ee Mungu, mawazo yako ni makubwa sana; hayawezi kabisa kuhesabiwa. Ningeyahesabu yangekuwa mengi kuliko muchanga. Hata ninapoamuka, ningali pamoja nawe. Heri, ee Mungu, ungewaua watu waovu! Heri wauaji wangeniondokea! Wanasema vibaya juu yako; wanasema maovu juu ya jina lako! Ee Yawe, ninawachukia wanaokuchukia; ninawazarau sana wale wanaokuasi! Waadui zako ni waadui zangu; ninawachukia kabisa kabisa. Unichunguze, ee Mungu, unijue moyo wangu, unipime, uyajue mawazo yangu. Uangalie kama mwenendo wangu ni mubaya, uniongoze katika njia ya milele. Kwa mukubwa wa waimbaji. Zaburi ya Daudi. Ee Yawe, uniokoe na watu wabaya, unikinge na watesaji wakali. Watu hao wanafikiri mabaya siku zote, wanaamusha ugomvi kila mara. Ndimi zao ni hatari kama za nyoka; ndani ya midomo yao kuna maneno ya sumu kama ya piri. Ee Yawe, unilinde na makucha ya wabaya; unikinge na watesaji wakali ambao wamepanga kuniangusha. Wenye kiburi wamenitegea mitego, wametandika kamba kama wavu, wameficha mitego katika njia wanikamate. Ninamwambia Yawe: “Wewe ni Mungu wangu.” Usikilize, ee Yawe, sauti ya ombi langu. Ee Yawe, Bwana wangu, mukombozi wangu mukubwa, umenikinga salama wakati wa vita. Ee Yawe, usiwape waovu vitu wanavyotaka, wala mipango yao mibaya usiifanikishe. Hao wanaonizunguka wanainua vichwa; uovu wa maneno yao uwapate wao wenyewe! Makaa ya moto yawaangukie; watumbukizwe katika mashimo, wasiinuke tena. Wanaosingizia wengine wasifanikiwe katika inchi; uovu uwapate watesaji wakali na kuwaangamiza bila kukawia! Ninajua kwamba Yawe anatetea wamasikini na kuwapatia wakosefu haki. Hakika watu wa haki watasifu jina lako; watu wa usawa watakaa kwako. Kwa mukubwa wa waimbaji: Zaburi ya Daudi. Ninakulilia, ee Yawe, ukuje haraka kunisaidia! Usikilize sauti yangu wakati ninapokuita! Upokee maombi yangu kama ubani; ninapoinua mikono yangu kwako, unikubali kama sadaka ya magaribi. Ee Yawe, ulinde kinywa changu, uweke mulinzi kwenye mulango wa kinywa changu. Unikinge nisielekee kufanya mabaya, nisijishugulishe na matendo maovu, nisijiunge na watu wanaotenda mabaya, wala nisishiriki hata kidogo katika karamu zao. Afazali mutu mwema anipige kwa kunionya; lakini sikubali hata kidogo kusifiwa na wabaya, maana ninaomba siku zote juu ya maovu yao. Wakubwa wao watakapopondwa juu ya mawe, ndipo watatambua kwamba maneno yangu yalikuwa mazuri. Mifupa yao itatawanywa kwenye midomo ya kuzimu kama kuni zilizopasuliwa vipandevipande! Lakini mimi ninakutegemea, ee Yawe, Mungu wangu; ninakimbilia kwako, usiniache katika hatari. Unikinge na mitego waliyonitegea, uniepushe na wavu wa hao watu waovu. Waovu wanaswe katika mitego yao wenyewe, wakati mimi ninaponyoka. Mashairi ya Daudi alipokuwa ndani ya pango. Ninamulilia Yawe kwa sauti kubwa, ninamusihi Yawe kwa sauti kubwa. Ninamutolea malalamiko yangu, ninamwelezea taabu zangu. Roho yangu inaporegea kabisa, yeye yuko, anajua mwenendo wangu. Waadui wamenitegea mitego katika njia ninayopita. Nikiangalia kwa kuume kwangu na kungojea, ninaona hakuna mutu wa kunisaidia; sina tena nafasi ya kukimbilia, hakuna mutu anayenijali. Ninakulilia wewe, ee Yawe! Wewe ni kimbilio langu; wewe ni hitaji langu lote katika inchi ya wenye uzima. Usikilize kilio changu, maana nimetabanika sana; uniokoe kutoka watesaji wangu, maana wamenizidi nguvu. Uniondoe humu katika kifungo, kusudi nipate kukushukuru, nikijiunga na watu wa haki kwa sababu ya vyote ulivyonitendea. Zaburi ya Daudi. Usikie maombi yangu, ee Yawe! Ulitegee ombi langu sikio, maana wewe ni mwaminifu; unijibu kwa sababu ya haki yako. Usinitie katika hukumu mimi mutumishi wako, maana hakuna yeyote anayekuwa mwenye haki mbele yako. Waadui zangu wamenifuatilia, wameniangusha chini kabisa, wameniikalisha katika giza kama mutu aliyekufa zamani. Roho yangu imeregea kabisa; moyo wangu unaugua. Ninakumbuka siku za zamani, ninafikiri juu ya yote uliyotenda, ninawazawaza matendo yako. Ninakunyooshea mikono yangu. Ninakuhitaji wewe, kama inchi kavu inavyohitaji mvua. Ee Yawe, unijibu haraka; maana roho yangu imeregea kabisa! Usinigeuzie mugongo, kusudi nisikuwe kama wale wanaoshuka katika shimo la wafu. Kila asubui unionyeshe wema wako, maana ninakutumainia. Unifundishe mwenendo wa kufuata, maana ninakutolea moyo wangu. Uniokoe, ee Yawe, kutoka waadui zangu, maana ninakimbilia kwako. Unifundishe kutimiza mapenzi yako, maana wewe ni Mungu wangu! Roho wako muzuri aniongoze katika njia sawa. Ulinde uzima wangu, ee Yawe, kwa ajili ya jina lako, uniondoe katika taabu, kwa ajili ya haki yako. Kwa ajili ya wema wako uwakomeshe waadui zangu, uwaangamize wote wanaonitesa, maana mimi ni mutumishi wako. Zaburi ya Daudi. Atukuzwe Yawe, yeye ni: nguvu yangu, yule anayeizoeza mikono yangu kupigana vita na kuvifundisha vidole vyangu kugombana, rafiki yangu wa kweli, kimbilio langu, upango wangu, mukombozi wangu, ngao yangu, yule anayenilinda, yule anayeshinda mataifa na kuyaweka chini yangu. Ee Yawe, mutu ni nini hata umujali? Mwanadamu ni nini hata ufikiri juu yake? Mwanadamu ni kama pumzi tu; siku zake zinapita kama kivuli. Uinamishe mbingu zako, ee Yawe, ushuke chini! Uiguse milima, nayo itoe moshi! Upige umeme, uwasambaze waadui; upige mishale yako, uwakimbize! Unyooshe mukono wako kutoka juu, uniopoe katika maji haya mengi, uniokoe kutoka makucha ya wageni ambao wanasema maneno ya uongo na kunyoosha mukono kwa kushuhudia uongo. Ee Mungu, nitakuimbia wimbo mupya; nitakupigia kinubi cha nyuzi kumi, wewe unayewapa wafalme ushindi, unayemwokoa mutumishi wako Daudi! Uniokoe kutoka upanga wa waadui wakali, uniokoe kutoka makucha ya wageni, ambao wanasema maneno ya uongo, wanaonyoosha mukono kwa kushuhudia uongo. Katika ujana wao, wana wetu wakuwe kama mimea iliyostawi vizuri; nao wabinti wetu wakuwe wazuri kama nguzo zilizochongwa kwa kupamba nyumba ya kifalme. Gala zetu zijae mavuno ya kila aina. Kondoo wetu katika mbuga wazae maelfu na maelfu. Ngombe wetu wakuwe na afya na nguvu, kusitokwe mimba wala kukosa kuibeba. Kusikuwe tena kilio katika mitaa yetu. Heri taifa ambalo limejaliwa hayo! Heri taifa ambalo Yawe ndiye Mungu wao! Wimbo wa sifa wa Daudi. Nitakutukuza, ee Mungu wangu na mufalme wangu; nitalitukuza jina lako kwa milele na milele. Nitakutukuza kila siku; nitalisifu jina lako kwa milele na milele. Yawe ni mukubwa, anastahili sifa nyingi; ukubwa wake hauwezi kuchunguzika. Sifa za matendo yako zitaelezwa kwa kizazi hata kizazi, watu watatangaza matendo yako makubwa. Nitasema juu ya utukufu na mamlaka yako, nitafikiri juu ya matendo yako ya ajabu. Watu watatangaza ukubwa wa matendo yako ya ajabu, nami nitatangaza ukubwa wako. Watatangaza sifa za uzuri wako mwingi, na kuimba juu ya haki yako. Yawe ni mwenye huruma na rehema; yeye hakasiriki upesi, amejaa wema. Yawe ni muzuri kwa wote, ni mwenye huruma kwa viumbe vyake vyote. Viumbe vyako vyote vitakushukuru, ee Yawe, nao waaminifu wako watakutukuza. Watasema juu ya utukufu wa ufalme wako, na kutangaza juu ya nguvu yako kubwa, kusudi kila mutu ajue matendo yako makubwa, na mamlaka ya ufalme wako wenye utukufu. Ufalme wako ni ufalme wa milele; mamlaka yako yanadumu vizazi vyote. Yawe ni mwaminifu katika ahadi zake zote, ni mwema katika matendo yake yote. Yawe anawashikilia wote wanaoanguka; anawainua wote waliogandamizwa. Viumbe vyote vinakutazamia, nawe unavipatia chakula chao kwa wakati wake. Unafumbua mukono wako kwa moyo safi, unatimiza mahitaji ya kila kiumbe kinachoishi. Yawe ni mwenye haki katika njia zake zote; ni mwema katika matendo yake yote. Yawe yuko karibu na wote wanaomwomba, wote wale wanaomwomba kwa uaminifu. Anajibia mahitaji yao wote wanaomwabudu; anasikia kilio chao na kuwaokoa. Yawe anawalinda wote wanaomupenda; lakini anawaangamiza waovu wote. Nitatangaza sifa za Yawe; viumbe vyote vilisifu jina lake takatifu, kwa milele na milele. Haleluia! Ee nafsi yangu, umusifu Yawe! Nitamusifu Yawe maisha yangu yote; nitamwimbia Mungu wangu muda wote nitakapoishi. Musiwategemee wakubwa wa dunia; hao ni wanadamu tu, hawawezi kuokoa. Mwanadamu akitoa pumzi yake ya mwisho, anarudi katika mavumbi alimotoka, na hapo mipango yake yote inatoweka. Heri mutu anayesaidiwa na Mungu wa Yakobo, mutu anayemutumainia Yawe, Mungu wake, aliyeumba mbingu na dunia, bahari na vyote vinavyokuwa ndani yao. Yeye anashika ahadi yake milele. Yeye anawapatia wanaoonewa haki yao, anawapa wenye njaa chakula. Yawe anawapa wafungwa uhuru, anawafungua vipofu macho. Yawe anawainua waliogandamizwa; anawapenda watu wa haki. Yawe anawalinda wageni, anawasaidia wajane na wayatima; lakini anaharibu mipango ya waovu. Yawe anatawala milele. Mungu wako, ee Sayuni, ni mufalme kwa vizazi vyote! Haleluia! Haleluia! Kweli ni vizuri kumwimbia Mungu wetu sifa! Inapendeza na inastahili kumwimbia. Yawe anajenga tena Yerusalema; anawarudisha Waisraeli waliopelekwa katika uhamisho. Anawaponyesha waliovunjika moyo; na kuwatunza vidonda vyao. Anakadirisha hesabu ya nyota, na kupanga kila moja jina. Bwana wetu ni mukubwa, ana nguvu nyingi; maarifa yake hayana kipimo. Yawe anawashikilia wanyenyekevu, lakini anawaangusha waovu katika mavumbi. Mumwimbie Yawe nyimbo za shukrani, mumupigie Mungu wetu kinubi! Yeye anafunika anga kwa mawingu, anaitayarishia inchi mvua, na kuchipukiza nyasi kwenye vilima. Anawapa nyama chakula chao, na kulisha vitoto vya kibombobombo vinapomulilia. Yeye hafurahii nguvu za farasi, wala hapendezwi na ushujaa wa waaskari; lakini anapendezwa na watu wanaomuheshimu, ndio wanaotegemea wema wake. Umusifu Yawe, ee Yerusalema! Umusifu Mungu wako, ee Sayuni! Maana yeye alikaza vifungio vya milango ya kuta zako, anawabariki watu wanaokuwa ndani yako. Analeta amani katika eneo lako; anakushibisha kwa ngano safi kabisa. Yeye anatuma amri yake katika dunia, na neno lake linafikia shabaha yake kwa haraka. Ananyesha teluji inayoangaa kama pamba, anasambaza umande kama majivu. Anaangusha mvua ya mawe kama makokoto, hakuna anayeweza kuvumilia baridi anayoituma. Anapoamuru, hayo mawe yanayeyuka; anapovumisha upepo, maji yanatiririka. Anatoa ujumbe wake kwa wazao wa Yakobo, nayo masharti na maagizo yake kwa Waisraeli. Lakini hakuyatendea hivyo mataifa; wao hawajui maagizo yake. Haleluia! Haleluia! Mumusifu Yawe kutoka mbinguni, mumusifu kutoka huko juu mbinguni. Mumusifu enyi wamalaika wake wote, mumusifu enyi jeshi lake lote. Mumusifu enyi jua na mwezi, mumusifu enyi nyota zote zinazoangaza. Mumusifu enyi mbingu za juu, na maji yanayokuwa juu ya mbingu. Vyote visifu jina la Yawe, maana yeye aliamuru, na vyote vikakuwa. Yeye aliviweka nafasi yao kwa milele, kwa amri ambayo haiwezi kuvunjika. Mumusifu Yawe tokea katika dunia; enyi nyoka wakubwa wa bahari na mashimo ya bahari, mumusifu. Mumusifu, enyi moto, mvua ya mawe na teluji, upepo wenye zoruba unaotimiza amri yake! Mumusifu, enyi milima na vilima, miti ya matunda na ya mierezi! Mumusifu, enyi nyama wa pori na wa kufugwa, viumbe vinavyotambaa na ndege wote! Mumusifu, enyi wafalme na mataifa yote; waongozi na watawala wote katika dunia! Mumusifu, enyi vijana wanaume na wabinti; wazee wote na watoto! Wote musifu jina la Yawe, maana jina lake peke yake linatukuzwa; utukufu wake unapita dunia na mbingu. Amewapa watu wake nguvu; nayo heshima kwa watu wote waaminifu, ndio watu wa Israeli wapendwa wake. Haleluia! Haleluia! Mumwimbie Yawe wimbo mupya; mumusifu katika kusanyiko la waaminifu! Umufurahie Muumba wako, ee Israeli; ninyi wakaaji wa Sayuni, mumushangilie mufalme wenu. Mulisifu jina lake mukicheza, mumwimbie kwa ngoma na zeze. Maana Yawe anapendezwa na watu wake; yeye anawaheshimisha wanyenyekevu kwa kuwapa ushindi. Waaminifu wafurahi, wakitukuza Mungu, hata wanapolala. Wamusifu Mungu kwa sauti kubwa, wakishika panga zenye kukata pande mbili, wawalipize mataifa kisasi, wawaazibu watu; wawafunge wafalme wao kwa minyororo, nao waongozi wao kwa vifungio vya chuma, kusudi wawaazibu sawa ilivyoamuriwa! Na huu ndio utukufu wa waaminifu wa Mungu. Haleluia! Mumusifu Mungu katika pahali pake patakatifu, mumusifu juu mbinguni kwenye uwezo wake! Mumusifu kwa sababu ya matendo yake makubwa, mumusifu kwa ajili ya utukufu wake mukubwa! Mumusifu kwa mulio wa baragumu, mumusifu kwa zeze na kinubi! Mumusifu kwa ngoma na michezo, mumusifu kwa filimbi na kinanda! Mumusifu kwa matoazi ya sauti kubwa, mumusifu kwa matoazi yenye kuvuma sana! Kila kiumbe chenye uzima kimusifu Yawe! Mumusifu Yawe! Hizi ni mezali za Solomono mwana wa Daudi mufalme wa Israeli. Zitawawezesha watu kujua hekima na mafundisho, na kufahamu misemo yenye maana kubwa. Zitawafundisha watu matendo ya hekima, haki, usawa, na sheria ya Mungu. Zitawaerevusha wajinga, zitawapa vijana maarifa na akili. Mwenye hekima akizisikiliza, zitamwongezea elimu; na mwenye ufahamu zitamupatia ujuzi. Wataweza kuelewa mezali na maana iliyofichwa, watayaelewa maneno ya wenye hekima na vitendawili vyao. Kumwogopa Yawe ni musingi wa maarifa, lakini wapumbafu wanazarau hekima na mafundisho. Mwana wangu, sikiliza mafundisho ya baba yako, wala usizarau mashauri ya mama yako; hayo yatakupamba kilemba cha neema juu ya kichwa chako, kama mukufu katika shingo yako. Mwana wangu, usikubali kushawishiwa na wenye zambi. Wakisema: “Twende kuvizia mutu na kumwua; kuja tuwashambulie wasiokuwa na kosa! Tutawameza wakiwa wazima kama kuzimu, watakuwa kama wale wanaoshuka katika shimo. Tutajitwalia mali zote za bei kali, tutazijaza nyumba zetu vitu tulivyonyanganya. Kuja na ushirikiane nasi, vyote tutakavyopata tutagawanyana.” Wewe mwana wangu usiandamane nao, uzuie muguu wako usifuatane nao. Maana wao wako mbio kutenda maovu, haraka zao zote ni za kumwanga damu. Mutego unaotegwa na ndege akiona, mutego ule unategwa bure. Wao wanavizia na kujiangamiza wao wenyewe, wanatega mutego wa kujinasa wao wenyewe. Ndizo njia za wanyanganyi; maisha yao yananyanganywa. Hekima inapiga kelele katika barabara, inaita kwa sauti kubwa katika viwanja; inaita kwenye masanganjia, inaita kwenye milango ya muji: “Enyi wajinga! Mpaka wakati gani mutapenda kuwa wajinga? Mpaka wakati gani wenye kuzarau watafurahia mazarau yao, na wapumbafu kuchukia maarifa? Musikilize maonyo yangu; nitawamiminia mawazo yangu, nitawajulisha maneno yangu. “Nimewaita nanyi mumekataa kusikiliza, nimewanyooshea mukono mukuje nanyi hamukujali, mumetupilia mashauri yangu yote, mumezarau maonyo yangu. Halafu mutaniita lakini sitaitika; mutanitafuta kwa bidii lakini hamutanipata. “Muliyachukia maarifa, wala hamukuchagua kumwogopa Yawe, mulikataa shauri langu, mukazarau maonyo yangu yote. Basi, mutakula matunda ya mienendo yenu, mutageukiwa na mashauri yenu wenyewe. Maana wajinga wanajiua kwa kiburi chao, wapumbafu wanajiangamiza kwa kufanikiwa kwao. Lakini mutu anayenisikiliza atakaa salama, atatulia bila kuogopa mabaya.” Mwana wangu, ukikubali maneno yangu, na kushika maagizo yangu, ukitega sikio lako kwa kusikiliza hekima, na kuelekeza moyo wako upate ufahamu, ukiomba upewe akili, ukisihi upewe ufahamu, ukitafuta hekima kama feza, na kuitaka kama hazina iliyofichwa, utaelewa maana ya kumwogopa Yawe, utafahamu maana ya kumujua Mungu. Maana Yawe anawapa watu hekima; katika kinywa chake kunatoka maarifa na ufahamu. Anawawekea watu wa usawa akiba ya hekima safi, yeye ni ngao kwa watu wanaoishi kwa ukamilifu. Analinda mienendo ya watu wanaofuata sheria yake, na kuchunga njia za waaminifu wake. Ukinisikiliza, utafahamu haki, usawa, na kufuata sheria ya Mungu; utafahamu kila njia nzuri. Maana hekima itaingia ndani ya moyo wako, na maarifa yatapendeza nafsi yako. Hekima itakulinda, ufahamu utakuchunga; vitakuepusha na njia ya uovu, na watu wa maneno mapotovu, watu wanaoacha njia zenye kunyooka kwa kufuata njia za giza, watu wanaofurahia kutenda maovu na kupendezwa na upotovu wa maovu, watu ambao mienendo yao imepotoka, nazo njia zao haziaminiki. Utaepukana na mwanamuke mwasherati, mwanamuke kahaba wa maneno matamu, mwanamuke anayemwacha mwenzake wa ujana wake, na kusahau agano la Mungu wake. Nyumba yake inaelekea kifo, njia zake zinakwenda kuzimu. Yeyote anayemwendea harudi hata kidogo, wala harudilii tena njia ya uzima. Kwa hiyo utafuata mufano wa watu wazuri, na kufuata mienendo ya wenye haki. Maana watu wa usawa watarizi inchi, na watu wakamilifu watadumu ndani yake. Lakini waovu wataondolewa katika inchi, na watu wabaya watangolewa toka ndani yake. Mwana wangu, usisahau mafundisho yangu, lakini kwa moyo wako ushike amri zangu. Maana vitakupa wingi wa siku, maisha marefu na fanaka kwa wingi. Wema na uaminifu zisitengane nawe. Uvifunge katika shingo lako; uviandike ndani ya moyo wako. Hivyo utakubaliwa na kusifiwa, mbele ya Mungu na mbele ya wanadamu. Umutumainie Yawe kwa moyo wako wote, wala usitegemee akili zako mwenyewe. Umutambue Mungu katika kila kitu unachofanya, naye atasawanisha njia zako. Usijione wewe mwenyewe kuwa mwenye hekima; umwogope Yawe na kujiepusha na uovu. Hiyo itakuwa dawa kwa mwili wako, na kitu cha kutuliza mifupa yako. Umuheshimu Yawe kwa mali yako, na kwa malimbuko ya mazao yako yote. Kwa hiyo gala zako zitajaa ngano, na mitungi yako itafurika na divai mupya. Mwana wangu, usizarau azabu ya Yawe, wala usiuzike kwa maonyo yake; maana Yawe anaonya yule anayemupenda, kama vile baba anavyomwonya mwana wake mupenzi. Heri mutu anayetambua hekima, mutu yule anayepata ufahamu. Hekima ni bora kuliko feza, ina faida kuliko zahabu. Hekima ni ya maana sana kuliko mawe ya bei kali, hakuna kitu unachotamani kinachoweza kulingana nayo. Itakupa maisha marefu, mali na heshima. Njia zake ni za kupendeza, zote zinaelekea kwenye amani. Hekima ni muti wa uzima kwa wote wanaoipata; wana heri wote wanaoshikamana nayo. Kwa hekima Yawe aliweka misingi ya dunia, kwa akili aliziimarisha mbingu. Kwa maarifa yake vilindi vilipasuka, na mawingu yakadondosha umande. Mwana wangu, shika hekima safi na akili; usiviache vitoweke mbele ya macho yako, navyo vitakuwa uzima katika nafsi yako, na pambo zuri katika shingo lako. Halafu utaweza kwenda zako kwa usalama, wala muguu wako hautajikwaa. Unapolala, hautakuwa na hofu, utapata usingizi muzuri. Usiogope juu ya tisho la rafla, wala shambulio kutoka kwa waovu, maana Yawe ndiye atakayekutegemeza, atakuepusha usipate kunaswa katika mutego. Usimunyime mutu anayehitaji musaada, ikiwa una uwezo wa kufanya hivyo. Usimwambie jirani yako “Kwenda na urudie kesho, halafu nitakupatia” wakati wewe unaweza kumupa anachohitaji leo. Usipange maovu juu ya jirani yako anayeishi karibu nawe bila wasiwasi. Usigombane na mutu bila sababu, ikiwa hajakuzuru kwa lolote. Usimwonee wivu mutesaji, wala usiige mwenendo wake. Maana waovu ni chukizo kwa Yawe, yeye anawafanya watu wa usawa kuwa warafiki zake. Yawe analaani nyumba za waovu, lakini anabariki makao ya wenye haki. Yeye anazarau wenye mazarau, lakini anakubali wanyenyekevu. Wenye hekima watavuna heshima, lakini wapumbafu watapata haya. Wana wangu, musikilize maadibisho ya baba yenu, mutege sikio mupate kuwa na akili. Maana ninawapa kanuni zuri, musikatae mafundisho yangu. Mimi vilevile nilikuwa mutoto kwa baba yangu, nilikuwa mupole, kipenzi cha mama yangu. Baba yangu alinifundisha hiki: “Shika kwa moyo maneno yangu, shika amri zangu nawe utaishi. Ujipatie hekima, ujipatie ufahamu; usisahau wala kuzarau maneno yangu. Usimwache hekima, nayo itakutunza; umupende, nayo itakulinda. Jambo la musingi ni kujipatia hekima; toa vyote unavyokuwa navyo ujipatie akili. Shikamana sana na hekima, nayo itakutukuza; ukiishikilia itakupa heshima. Itavalisha kilemba cha neema kwenye kichwa chako, atakupa taji lenye utukufu.” Mwana wangu, sikia na kupokea maneno yangu, kusudi upate kuwa na miaka mingi ya kuishi. Nimekufundisha njia ya hekima, nimekuongoza katika njia ya usawa. Ukitembea hatua zako hazitazuizwa, wala ukikimbia hautajikwaa. Shika mafundisho ya hekima na usimwache iponyoke, uishike kwa uangalifu maana ni uzima wako. Usijiingize katika njia ya waovu, wala usifuate mwenendo wa watu wabaya. Epuka njia hiyo wala usiikaribie; ujiepushe nayo, uende zako. Waovu hawalali hata kidogo wasipotenda uovu; hawapati usingizi wasipomukwaza mutu. Maana uovu ndicho chakula chao, mateso makali ndiyo divai yao. Njia ya wenye haki ni kama mwangaza wa asubui mapema, ambao unaangaza zaidi na zaidi hata muchana kamili. Lakini njia ya waovu ni kama giza nene, hawajui kinachowafanya wajikwae. Mwana wangu, sikia kwa uangalifu maneno yangu, utegee sikio masemi yangu. Usiyaache yatoweke mbele ya macho, uyafunge ndani ya moyo wako. Maana hayo ni uzima kwa mutu anayeyapata, ni dawa kwa mwili wake wote. Linda moyo wako kwa uangalifu wote, maana mule munatokea chemichemi za uzima. Tenga mbali nawe luga potovu; wala midomo yako isiseme maneno madanganyifu. Uyaelekeze macho yako mbele sawasawa, kope zako zipige sawasawa. Chunguza sana njia utakayopitia, na hatua zako zote zitakuwa kamili. Usigeukie kuume wala kushoto; epusha muguu wako mbali na uovu. Mwana wangu, sikia hekima yangu, tega sikio usikie elimu yangu. Kwa hiyo, utaweza kulinda akili, na kinywa chako kitashika maarifa. Midomo ya mwanamuke mupotovu ni mitamu kama asali, maneno yake ni laini kuliko mafuta; lakini kwa mwisho ni michungu kama nyongo, ni mikali kama upanga wenye makali ngambo mbili. Miguu yake inaelekea chini kwenye kifo, hatua zake zinaenda kuzimu. Yeye haijali njia ya uzima, njia zake ni za kutangatanga, wala hajui. Sasa enyi wana wangu, musikilize, wala musisahau maneno ya kinywa changu. Uepushe njia yako mbali naye, wala usiukaribie mulango wa nyumba yake, kusudi usiwape wengine heshima yako, na watenda mabaya miaka yako, wageni wasipate kushibishwa kwa mali yako, na faida ya kazi yako kuishia katika nyumba ya mugeni. Kwa mwisho wa maisha yako utaomboleza, wakati mwili wako utakapoangamizwa. Kwa hiyo utasema: “Kwa nini nilichukia mafundisho? Kwa nini nilizarau ndani ya moyo wangu? Sikusikiliza sauti ya walimu wangu, wala kuwategea sikio wale walionifundisha. Nikakuwa karibu ya kuangamia kabisa katika kusanyiko na mukutano wa watu.” Kunywa maji ya birika lako mwenyewe, maji yanayobubujika katika kisima chako mwenyewe. Kwa nini chemichemi zako zitawanywe mbali, na vijito vya maji katika barabara? Hiyo ni yako wewe mwenyewe, wala usiwashirikishe watu wengine. Chemichemi yako ibarikiwe, umufurahie muke uliyemwoa ukiwa kijana. Ni muzuri kama pongo, anapendeza kama paa. Mapenzi yake yakufurahishe kila wakati, uvutwe siku zote na mapendo yake. Mwana wangu, kwa nini kutekwa na mwanamuke mwasherati? Kwa nini kukumbatia mwanamuke mugeni katika kifua? Maana mwenendo wa kila mutu ni wazi mbele ya Yawe; yeye anachunguza njia zake zote. Mutu mwovu ananaswa kwa uovu wake mwenyewe; anakamatwa na vifungo vya zambi yake mwenyewe. Yeye anakufa kwa ajili ya ukosefu wa mafundisho, anaangamia kwa sababu ya upumbafu wake mukubwa. Mwana wangu, kama umejitolea kubeba deni ya mwenzako, ikiwa umetoa ahadi yako kwa ajili ya mutu yule, ikiwa umejifunga kwa maneno yako mwenyewe, utajinasa kwa ahadi uliyofanya; ujue kwamba uko chini ya mamlaka ya mwenzako, lakini mwana wangu, ukitaka kujiokoa, basi fanya hivi: umwendee mutu yule mara moja, umusihi akupe uhuru wako. Usiache macho yako yapate usingizi, wala kope za macho yako zisinzie. Ujiokoe kwa kujitoa katika mutego ule, ujiponyeshe kama vile paa au ndege anayemutoroka mwindaji. Ewe muvivu! Kwenda kuchunguza siafu, fikiri juu ya namna yake ya kuishi upate hekima. Siafu hana kiongozi, mukubwa, wala mutawala; lakini anajiwekea chakula wakati wa kipwa, anajikusanyia akiba wakati wa mavuno. Ewe muvivu, utalala pale mpaka wakati gani? Utaamuka wakati gani katika usingizi wako? Unasema: “Acha nilale kidogo tu, acha nisinzie kidogo! Uniache nikunje mikono nipumzike kidogo!” Wakati ule umasikini utakushambulia kama munyanganyi, ukosefu utakufuata kama mwizi mwenye silaha. Mutu mwovu, mutu asiyefaa kitu, anatangatanga akisema maneno mapotovu. Anakonyeza jicho kwa kuwakosesha wengine, anaparuza kwa miguu na kufanyia watu kitambulisho kwa vidole. Akiwa amejaa mabaya ndani ya moyo, anatunga maovu. Anaamusha ugomvi kila pahali. Kutokana na hayo hasara itamupata kwa rafla; kwa rafla atapondekana vibaya wala hatapata kupona. Kuna vitu sita Yawe anavyochukia, hata saba ambavyo ni chukizo kwake: Macho ya kiburi, ulimi mudanganyifu, mikono inayoua wasiokuwa na kosa, moyo unaopanga mipango miovu, miguu inayokuwa mbio kutenda maovu, mushuhuda wa uongo anayesema uongo, na mutu anayechochea fitina kati ya wandugu. Mwana wangu, shika amri za baba yako, wala usisahau mashauri ya mama yako; uyaweke siku zote ndani ya moyo, uyafunge katika shingo lako. Yatakuongoza katika njia yako, yatakulinda wakati unapolala, yatakushauria unapoamuka. Maana amri hizi ni taa, na shauri hilo ni mwangaza. Maonyo hayo ya mafundisho ni njia ya uzima. Yatakulinda mbali na mwanamuke mubaya, yatakuepusha na maneno matamu ya mwanamuke mugeni. Usimutamani mwanamuke yule kwa uzuri wake, wala usikubali kunaswa kwa kope za macho yake. Mutu anapoteza kipande cha mukate kwa kahaba, lakini mwanamuke muzinzi atapoteza uzima wako wote. Mutu anaweza kuweka moto kwenye kifua chake na nguo zake zikose kuungua? Mutu anaweza kukanyaga makaa ya moto na miguu yake ikose kuungua? Ndivyo mwanaume anayelala na muke wa mwenzake anavyokuwa; yeyote anayemugusa mwanamuke yule hataacha kuazibiwa. Watu hawamuzarau sana mutu akiiba kwa sababu ya njaa, lakini akipatikana anapaswa kulipa mara saba, tena atatoa mali yote anayokuwa nayo. Anayezini hana akili kabisa; anajiangamiza yeye mwenyewe. Atapata vidonda na mazarau; haya atakayopata haitatoka juu yake. Maana wivu wa mume unamufanya kuwa mukali kabisa; wakati atakapolipiza kisasi hana kitu cha kuhurumia. Hatakubali malipo yoyote; wala kutulizwa na zawadi zako nyingi. Mwana wangu, ushike maneno yangu, uchunge amri zangu. Ufuate amri zangu nawe utaishi; ulinde mafundisho yangu kama mboni ya jicho lako. Uyafunge kwenye vidole vyako; uyaandike ndani ya moyo wako. Uambie Hekima: “Wewe ni dada yangu”, na Akili: “Wewe ni rafiki yangu”. Vitakulinda mbali na mwanamuke mubaya, vitakuepusha na maneno matamu ya mwanamuke mugeni. Siku moja katika dirisha ya nyumba yangu, nilichungulia inje kupitia nyavu za dirisha, nikawaona vijana wengi wajinga, na hasa mumoja aliyekuwa mupumbafu. Huyo alikuwa akitembea kwenye barabara ile, karibu na pahali mwanamuke mumoja alipoishi. Basi akashika njia inayokwenda kwa mwanamuke yule. Ilikuwa karibu wakati wa magaribi, giza na usiku vilikuwa vimeanza kuingia. Kijana akakutana na yule mwanamuke; alivaa kama kahaba, mwenye ukorofi. Alikuwa mwanamuke wa makelele na mwenye kiburi; miguu yake haitulii ndani ya nyumba: mara katika barabara, mara katika soko, pembeni ya njia hakosekani akivizia. Alimukumbatia kijana yule na kumubusu, na kwa maneno matamu, akamwambia: “Ilinipasa kutoa sadaka zangu; leo hii nimekamilisha naziri yangu. Ndio maana nimetoka kwa kukupokea, nimekutafuta kwa hamu nikakupata. Nimetandika kitanda changu vizuri, kwa blanketi za rangi za kitani kutoka Misri. Nimekinyuzia marasi, manemane, udi na mudalasini. Kuja! Tufanye mapenzi mpaka asubui; kuja tujifurahishe kwa mapenzi. Mume wangu hayuko ndani ya nyumba, amekwenda safari ya mbali. Amepeleka mufuko wa feza, hatarudi mbele ya mwandamo wa mwezi.” Alimushawishi kwa maneno mengi ya kubembeleza; kijana akashawishiwa kwa maneno yake matamu. Naye akamufuata yule mwanamuke moja kwa moja, kama ngombe anayekwenda kuchinjwa, kama mupambafu anayefungwa na kwenda kuazibiwa. Hakutambua kwamba maisha yake yako katika hatari, mpaka alipojikuta amekuwa kama amechomwa mushale ndani ya moyo, amekuwa kama ndege aliyerukia ndani ya wavu. Sasa wana wangu, munisikilize; mutege sikio kwa maneno ya kinywa changu. Musikubali kuongozwa na mwanamuke kama yule, wala musipitepite katika mapito yake. Maana amewaangusha wanaume wengi; ni wengi sana wale aliowachinja. Nyumba yake ni njia ya kwenda kuzimu, ni pahali pa kuteremukia katika mauti. Musikilize! Hekima inaita! Akili inapiga kelele yake! Juu kwenye vilima karibu na njia na katika masanganjia ndipo ilipojiweka. Karibu na milango ya kuingilia katika muji, pahali wanapoingilia watu inaita kwa sauti: “Enyi watu wote, ninawaita ninyi! Wito wangu ni kwa ajili ya wanadamu. Enyi wajinga, mujifunze kuwa na akili; musikilize kwa uangalifu, enyi wapumbafu. Musikilize maana nitakachosema ni jambo la lazima; katika midomo yangu mutatoka mambo ya haki. Kinywa changu kitasema kweli mutupu; uovu ni chukizo katika midomo yangu. Kinywa changu kitasema maneno ya haki, hakuna udanganyifu wala upotevu katika midomo yangu. Kwa mutu mwenye ufahamu kila kitu ni wazi, kwa mwenye maarifa yote imesawanishwa. Chagua mafundisho yangu pahali pa feza; na maarifa pahali pa zahabu safi. “Hekima ina maana sana kuliko mawe ya bei kali; kitu chochote unachotamani hakiwezi kulingana nayo. Mimi Hekima nina ujuzi; nina maarifa na akili. Kumwogopa Yawe ni kuchukia uovu. Ninachukia kiburi, majivuno maisha mabaya, na luga mbaya. Nina uwezo wa kushauri na kuamua vizuri. Nina ufahamu na nina nguvu. Kwa musaada wangu watawala wanatawala na wakubwa wanaagiza kwa haki. Kwa musaada wangu viongozi wanaongoza na wakubwa wanaamua. Ninawapenda wale wanaonipenda; wanaonitafuta kwa bidii wananipata. Utajiri na heshima viko kwangu, mali ya kudumu na fanaka. Matunda yangu ni mazuri kuliko zahabu safi, na faida yangu inashinda ya feza bora. Ninatembea katika njia ya haki; ninafuata sheria ya Mungu. Ninawatajirisha wale wanaonipenda, ninajaza tele hazina za wanaonipenda. “Yawe aliniumba kwa mwanzo wa kazi yake, zamani za kale mbele ya kuumbwa kwa kitu chochote. Nilifanywa kwa mwanzo wa nyakati, nilikuwa niko mbele ya dunia kuanza. Nilizaliwa mbele ya vilindi vya bahari, mbele ya chemichemi zinazobubujika maji. Nilizaliwa mbele milima na vilima havijaumbwa, mbele Mungu hajaumba dunia na mashamba yake, wala chembe za kwanza za mavumbi ya dunia. Nilikuwa niko wakati alipoweka mbingu, wakati alipofanya muviringo juu ya bahari; wakati alipoimarisha mawingu mbinguni, alipofanya imara chemichemi za bahari, wakati alipowekea bahari mupaka wake kusudi maji yake yasipate kuvunja amri yake, wakati alipoweka misingi ya dunia. Nilikuwa pamoja naye kama fundi wa kazi, nilikuwa furaha yake kila siku, nikishangilia mbele yake siku zote, nikifurahia dunia na wakaaji wake, na kupendezwa kuwa pamoja na wanadamu. “Sasa basi, wana wangu, munisikilize: heri wale wanaofuata njia zangu. Musikilize mafundisho mupate hekima, wala musiyakatae. Heri mutu anayenisikiliza, anayeikaa kila siku kwenye mulango wangu, anayekesha karibu na milango yangu. Anayenipata mimi amepata uzima, na upendeleo kutoka kwa Yawe. Asiyenipata anajizuru mwenyewe; wote wanaonichukia wanapenda kifo.” Hekima amejenga nyumba yake, nyumba yenye nguzo saba. Amechinja nyama wa karamu, divai yake ameitayarisha, ametandika meza yake. Amewatuma wajakazi wake katika muji waite watu kutoka kwenye vilele vya milima: “Yeyote anayekuwa mujinga akuje hapa!” Na yeyote anayekuwa mupumbafu unamwambia: “Kuja ukule chakula, na ukunywe divai niliyotengeneza. Achana na ujinga upate kuishi; fuata njia ya akili.” Anayemwonya mwenye kiburi anapata mazarau, anayekaripia mwovu anajiletea matusi. Usimwonye mwenye kiburi maana atakuchukia; umwonye mwenye hekima naye atakupenda. Umufundishe mwenye hekima naye atazidi kuwa na hekima; umufundishe mutu wa haki naye atazidi kuwa na elimu. Kumwogopa Yawe ni musingi wa hekima; na kumujua yule Mutakatifu ni kupata akili. Kwa musaada wangu mimi Hekima siku zako zitaongezwa; utaongezewa miaka mingi katika maisha yako. Kama una hekima, itakufaa wewe mwenyewe; kama ukiizarau, wewe mwenyewe utapata hasara. Mwanamuke mupumbafu ana kelele, hajui kitu wala hana haya. Anaikaa kitako kwenye mulango wa nyumba yake, anaweka kiti chake pahali pa juu katika muji, na kuwaita watu wanaopita katika njia, watu wanaokwenda kwenye shuguli zao: “Yeyote anayekuwa mujinga akuje hapa!” Na yeyote anayekuwa mupumbafu anamwambia: “Maji yaliyoibwa ni matamu sana; mukate unaokuliwa kwa siri ni muzuri sana.” Lakini mujinga hajui kwamba mule muna wafu, wageni wa mwanamuke yule wako chini katika kuzimu. Hizi ni mezali za Solomono: Mutoto mwenye hekima ni furaha ya baba yake; lakini mutoto mupumbafu ni huzuni ya mama yake. Mali iliyopatikana kwa njia mbaya haifai, lakini haki inaokoa mutu kutoka kifo. Yawe hawaachi wenye haki wapate njaa, lakini anapinga tamaa za waovu. Uvivu unasababisha umasikini, lakini mukono wa mutu wa bidii unajitajirisha. Mwenye akili anakusanya wakati wa mavuno. Kulala wakati wa kuvuna ni haya. Mwenye haki anajiletea baraka yeye mwenyewe, lakini kinywa cha mwovu kimesongwa na mateso makali. Mwenye haki anakumbukwa kwa baraka, lakini waovu watasahauliwa kabisa. Mwenye hekima anakubali maonyo, lakini mupumbafu anayesemasema mingi ataangamia. Anayeishi kwa ukamilifu anaishi salama, lakini anayepotosha maisha yake atagunduliwa. Anayekonyeza macho kwa nia mbaya analeta taabu, lakini anayeonya waziwazi analeta amani. Kinywa cha mwenye haki ni chemichemi ya uzima, lakini kinywa cha mwovu kimesongwa na mateso makali. Chuki inaleta ugomvi, lakini upendo unafunika makosa yote. Katika kinywa cha mwenye ufahamu kuna hekima, lakini wasiokuwa na akili watapigwa fimbo katika mugongo. Wenye hekima wanalinda maarifa, lakini kusemasema kwa mupumbafu kunaleta maangamizi haraka. Mali ya tajiri ndiyo kikingio chake. Umasikini wa masikini unamuletea maangamizi. Mushahara wa mutu wa haki ni uzima, lakini mapato ya mwovu ni katika zambi. Anayekubali kufundishwa anaelekea kwenye uzima, lakini anayekataa kuonywa amepotoka. Anayemuchukia mwingine kwa siri ni munafiki. Anayemusingizia mutu ni mupumbafu. Kwenye kuwa maneno mengi hakukosekani makosa, lakini aneyezuia ulimi wake ana akili. Maneno ya mwenye haki ni kama feza bora. Akili ya mutu mwovu haifai kwa kitu chochote. Maneno ya mwenye haki yanawafalia watu wengi, lakini wapumbafu wanakufa kwa kukosa akili. Baraka za Yawe ndizo zinazoleta utajiri. Juhudi za mutu haziongezi kitu. Kwa mupumbafu, kutenda maovu ni kama muchezo, lakini watu wenye akili wanafurahia hekima. Kitu mutu mwovu anachoogopa ndicho kitakachomupata, lakini kitu mwenye haki anachotamani ndicho atakachopewa. Upepo mukali unapopita na mwovu anatoweka, lakini mwenye haki anaimarishwa milele. Kama vile siki inavyokuwa kwa meno au moshi ndani ya macho, ndivyo muvivu anavyokuwa kwa bwana wake. Kumwogopa Yawe kunarefusha maisha, lakini miaka ya waovu itakuwa mifupi. Tumaini la mwenye haki linaleta furaha, lakini tazamio la mwovu linapotea bure. Yawe ni kimbilio la watu wenye mwenendo sawa, lakini ataangamiza watenda maovu. Wenye haki hawataondolewa katika inchi hata kidogo, lakini waovu hawatakaa katika inchi. Kinywa cha mwenye haki kinatoa mambo ya hekima, lakini ulimi wa mutu mubaya utakatwa mbali. Midomo ya wenye haki inajua mambo yatakayokubaliwa, lakini vinywa vya waovu vinasema tu maovu. Mizani danganyifu ni chukizo kwa Yawe, lakini matumizi ya vipimo vya haki ni furaha kwake. Kiburi kinazaa haya, lakini kwa watu wanyenyekevu kuna hekima. Ukamilifu wa watu wa usawa unawaongoza. Upotovu wa wadanganyifu unawaangamiza. Utajiri haufai kitu siku ya kasirani, lakini haki inaokoa kutoka kifo. Haki ya watu wakamilifu inanyoosha njia yao, lakini waovu wanaanguka kwa uovu wao wenyewe. Haki ya watu wa usawa inawaokoa na hatari, lakini wafitini wananaswa kwa tamaa zao wenyewe. Mwovu akikufa, tumaini lake nalo linatoweka. Tumaini la asiyemwogopa Mungu ni la bure. Mutu wa haki anaokolewa katika shida, na mwovu anaingia mule kwa pahali pake. Asiyemwogopa Mungu anaangamiza wengine kwa kinywa chake, lakini mwenye haki anaokolewa kwa maarifa yake. Watu wa haki wakipata fanaka, muji unashangilia. Waovu wakiangamia, watu wanapiga vigelegele. Muji unafanikishwa kwa baraka za watu wa usawa, lakini unaangamizwa kwa kinywa cha waovu. Anayemuzarau jirani yake hana akili; mutu mwenye ufahamu anakaa kimya. Anayepitapita akichongea anatoa siri, lakini anayeaminiwa anaficha siri. Pasipo uongozi taifa linaanguka; kwenye kuwa washauri wengi kuna usalama. Anayejitoa kulipia mugeni deni yake atajuta, lakini anayechukia mapatano yale ana usalama. Mwanamuke mwema anaheshimiwa; wanaume wenye nguvu wanatajirika. Mutu mwema anafaidika yeye mwenyewe, lakini mutu mukali anajiumiza mwenyewe. Faida mwovu anayopata ni ya uongo, lakini anayetenda mema, hakika atapata faida. Mutu anayekusudia kuwa mwenye haki ataishi, lakini anayechagua kutenda maovu atakufa. Wenye nia mbaya ni chukizo kwa Yawe, lakini wenye mwenendo mukamilifu ni furaha yake. Hakika mwovu hataepuka kuazibiwa, lakini wenye haki wataokolewa. Mwanamuke muzuri asiyekuwa na akili ni kama pete ya zahabu kwenye pua la nguruwe. Matazamio ya wenye haki yana matokeo mazuri; tamaa za waovu zinaleta kasirani. Kuna watu wanaotoa mali yao kwa wingi na kuzidi; lakini wachoyo wanazilinda na kuendelea katika umasikini. Mutu anayetoa kwa moyo safi atafanikishwa. Mutu anayekunywesha mwingine maji, naye atakunyweshwa. Watu wanamulaani mutu anayeficha ngano, lakini wanamutakia baraka mwenye kuiuzisha. Anayetafuta kutenda mazuri anapata upendeleo, lakini anayetafuta kutenda maovu atapatwa na maovu. Anayetegemea mali zake ataanguka, lakini mwenye haki atastawi kama jani bichi. Anayevunja nyumba yake, atavuna upepo. Mupumbafu atakuwa mutumwa wa wenye hekima. Tunda la mwenye haki ni muti wa uzima, na mwenye hekima anavuta watu. Ikiwa mwenye haki anapata malipo hapa katika dunia, hakika mwovu na mwenye zambi watalipwa! Anayependa mafundisho anapenda maarifa, lakini asiyependa kuonywa ni mujinga. Mutu muzuri anapata rehema za Yawe, lakini mwenye nia mbaya analaaniwa na Mungu. Mutu hawezi kudumu katika kutenda maovu, lakini hakuna kitu kinachoweza kumwangusha mutu wa haki. Muke mwema ni taji la utukufu kwa mume wake. Anayemupatisha mume wake haya ni kama kidonda ndani ya mifupa yake. Mawazo ya mwenye haki ni ya haki; mashauri ya mwovu ni ya udanganyifu. Maneno ya waovu shabaha yake ni kuua, lakini kinywa cha mutu wa usawa kinaokoa. Waovu wanaangamizwa na kutoweka kabisa, lakini jamaa ya wenye haki itasimama. Mutu anasifiwa kadiri ya hekima yake, lakini mwenye moyo wa mafikiri mabaya anazaruliwa. Afazali mutu wa chini anayejitegemea kuliko yule anayejitakia makubwa na kukosa chakula. Mutu mwenye haki anajali nyama wake, lakini huruma za waovu ni kutesa tu. Mulimaji mwenye bidii ana chakula tele, lakini anayefuata mambo yasiyofaa hana akili. Matumaini ya waovu yanaporomoka na kuharibika, lakini mutu mwenye haki anasimama imara. Mutu mwovu ananaswa kwa uongo wake mwenyewe, lakini mwenye haki anatoka katika taabu. Mutu anafanikiwa kutokana na maneno yake kama vile anavyopata matokeo ya kazi za mikono yake. Mupumbafu anaona njia yake kuwa sawa, lakini mwenye hekima anasikiliza shauri. Ujinga wa mupumbafu unajulikana mara moja, lakini mwerevu anazarau matusi. Musema kweli anatoa ushuhuda wa kweli, lakini mushuhuda wa uongo anasema udanganyifu. Maneno ya ovyo yanaumiza kama upanga, lakini kusema kwa mwenye hekima kunaponyesha kidonda. Ukweli unadumu milele, lakini uongo ni wa muda kidogo tu. Wanaopanga maovu wamejaa udanganyifu ndani ya moyo, lakini wanaokusudia mema wana furaha. Wenye haki hawapatwi na jambo lolote baya, lakini waovu wanapata hasara nyingi. Kinywa kinachosema uongo ni chukizo kwa Yawe, lakini watu waaminifu ni furaha yake. Mutu mwerevu anaficha maarifa yake, lakini wapumbafu wanatangaza upumbafu wao. Kuwa na bidii kutamupa mutu cheo, lakini uvivu utamufanya mutumwa. Wasiwasi ndani ya moyo inamukosesha mutu raha, lakini neno zuri linamuchangamusha. Mutu wa haki anaepuka uovu, lakini njia ya waovu inawapotosha wenyewe. Mwindaji muvivu hatapata anachowinda, lakini mwenye bidii atafanikiwa. Haki ni njia ya uzima, lakini uovu unaongoza katika kifo. Mutoto mwenye hekima anasikia maagizo ya baba yake, lakini mwenye kiburi hasikilizi maonyo. Mutu muzuri anapata uzuri kutokana na maneno yake, lakini mudanganyifu anaishi kwa kutesa kwa ukali. Anayechunga kinywa chake analinda maisha yake, mwenye midomo mirefu anajiletea maangamizi. Muvivu anatamani lakini hapati kitu chochote, wakati mwenye bidii anajaliwa kwa wingi. Mwenye haki anachukia uongo, lakini mwovu anatenda kwa kupatisha haya na mazarau. Haki inalinda wenye mwenendo sawa, lakini zambi inaangusha waovu. Kuna mutu anayejidai kuwa tajiri, kumbe hana kitu. Mwengine anajiona kuwa masikini wakati ana mali tele. Ukombozi wa uzima wa mutu ni mali yake, lakini masikini hana njia ya kujikomboa. Mwenye haki anaangaa kama vile taa inayowaka vizuri, lakini waovu ni kama taa inayozimika. Kiburi kinasababisha tu ugomvi, lakini kwa wanaokubali shauri jema kuna hekima. Mali ya harakaharaka inatoweka, lakini anayekusanya kidogokidogo ataiongeza. Tumaini la kungojangoja linaumiza moyo, lakini tazamio linalotimia ni musingi wa uzima. Anayezarau mashauri anajiletea maangamizi, lakini anayetii amri atapewa zawadi. Mafundisho ya wenye hekima ni chemichemi ya uzima; inamwezesha mutu kuepuka mitego ya kifo. Kuwa na akili kunaleta ukubali, lakini njia ya waovu ni ya taabu. Mwenye akili anatenda kila kitu kwa kufikiri, lakini mupumbafu anatembeza upumbafu wake. Mujumbe mubaya anawatumbukiza watu katika taabu, lakini mujumbe mwaminifu analeta amani. Umasikini na mazarau vinamupata yule asiyejali mafundisho, lakini mwenye kusikia maonyo anaheshimiwa. Ni jambo la kufurahisha unapopata kile unachotaka, kwa hiyo wapumbafu wanachukia kuepuka uovu. Anayeandamana na wenye hekima anapata hekima, lakini anayejiunga na wapumbafu atapata hasara. Wanaotenda zambi wanapatwa na hasara, lakini wenye haki wanafanikiwa. Mutu muzuri anawaachia wazao wake urizi, lakini mali ya mwenye zambi imelundikiwa wenye haki. Shamba la masikini linatoa mazao mengi, lakini linanyanganywa juu ya wale wanaopotosha haki. Asiyemwazibu mutoto wake hamupendi; lakini anayemupenda mwana wake atamwazibu kwa wakati. Mwenye haki yuko na chakula cha kumutoshelea, lakini tumbo la waovu linataabika kwa njaa. Mwanamuke mwenye hekima anajenga nyumba yake, lakini mupumbafu anaibomoa kwa mikono yake mwenyewe. Mwenye mwenendo sawa anamwogopa Yawe, lakini mupotovu anamuzarau Mungu. Ndani ya kinywa cha mupumbafu kunatokea maneno ya kiburi, lakini mwenye hekima analindwa na maneno yake. Bila ngombe wa kulima gala za mutu ni tupu. Mavuno mengi yanapatikana kwa nguvu ya ngombe wa kulima. Mushuhuda mwaminifu hasemi uongo, lakini asiyeaminiwa anabubujika uongo. Mwenye mazarau anatafuta hekima naye haipati, lakini mwenye akili anapata maarifa kwepesi. Ondoka pahali mupumbafu anapokuwa, maana pale anapokuwa hakuna maneno ya hekima. Hekima ya mwenye akili inamwonyesha njia yake, lakini upumbafu wa wapumbafu unawadanganya wenyewe. Wapumbafu wanafurahia zambi, lakini watu wa usawa wanapata rehema kwa Mungu. Moyo unajua uchungu wake wenyewe, wala mugeni hawezi kushiriki furaha yake. Nyumba ya mutu mwovu itabomolewa, lakini hema ya watu wa usawa itaimarishwa. Kuna njia inayozaniwa kuwa sawa, lakini kwa mwisho inaongoza kwenye kifo. Huzuni inaweza kufichwa katika kicheko; nyuma ya furaha kunakuja huzuni. Mutu mupotovu atavuna matunda ya mwenendo wake, naye mutu muzuri atapata malipo ya matendo yake. Mujinga anaamini kila kitu anachoambiwa, lakini mwenye akili anachunguza hatua zake zote. Mwenye hekima ni mwangalifu na anaepuka uovu, lakini mupumbafu hajizuizi wala hana uangalifu. Mwenye kuwaka hasira haraka anatenda kipumbafu, lakini mwenye akili ana uvumilivu. Wajinga wanarizi upumbafu, lakini wenye akili wanalipwa taji ya maarifa. Waovu watapiga magoti mbele ya watu wazuri, watu wabaya kwenye mulango wa wenye haki. Masikini anachukiwa hata na jirani yake, lakini tajiri ana warafiki wengi. Anayemuzarau jirani yake ni mwenye zambi, lakini ana heri yule anayekuwa mwema kwa masikini. Anayepanga kutenda maovu kweli anakosa! Wanaopanga kutenda mazuri watapata mema na uaminifu. Bidii katika kila kazi inaleta faida, lakini maneno matupu yanaleta umasikini. Mali ni taji ya utukufu wa wenye hekima, lakini ujinga ni kitambaa cha wapumbafu. Mushuhuda wa kweli anaokoa maisha, lakini musema uongo ni mudanganyifu. Anayemwogopa Yawe ana tumaini imara, na watoto wake watapata kimbilio salama. Kumwogopa Yawe ni chemichemi ya uzima inayowezesha mutu kuepuka mitego ya kifo. Utukufu wa mufalme ni wingi wa watu wake, lakini bila watu mutawala anaangamia. Mutu asiyekuwa mwepesi wa hasira ana akili nyingi, lakini anayekasirika upesi anaongeza upumbafu. Amani ndani ya roho inamupa mutu afya, lakini wivu inaozesha mifupa. Anayemutesa muzaifu anamutukana Muumba wake, lakini anayemwonea huruma mukosefu anamutukuza Mungu. Mwovu anaangamizwa kwa matendo yake maovu, lakini mwenye haki atapata usalama kwa uaminifu wake. Hekima iko ndani ya moyo wa mutu mwenye akili, lakini haipatikani hata kidogo ndani ya moyo wa mupumbafu. Haki inainua taifa, lakini zambi ni haya kwa taifa lote. Mufalme anapendezwa na mutumishi anayetenda kwa hekima, lakini hasira yake inawapata wanaotenda mambo yasiyofaa. Kujibu kwa upole kunatuliza hasira, lakini neno kali linachochea hasira. Ulimi wa mwenye hekima unaeneza maarifa, lakini watu wapumbafu wanamwanga maneno ya ujinga. Macho ya Yawe yanaona kila kitu, yanachunguza kibaya na kizuri. Ulimi mupole ni musingi wa uzima, lakini uovu wake unavunja moyo. Mupumbafu anazarau mafundisho ya baba yake, lakini anayekubali maonyo ni mwenye akili. Katika nyumba ya mwenye haki kuna wingi wa mali, lakini mapato ya waovu yanaleta hasara. Mudomo wa mwenye hekima unaeneza maarifa, lakini sivyo kwa mioyo ya wapumbafu. Sadaka ya waovu ni chukizo kwa Yawe, lakini maombi ya watu wa usawa yanamufurahisha Mungu. Mwenendo wa waovu ni chukizo kwa Yawe, lakini Mungu anawapenda wale wanaofuata mambo ya haki. Azabu kali ni kwa wanaoacha mwenendo mwema; yeyote anayechukia kuonywa atakufa. Ikiwa Yawe anajua kuzimu na shimo la kuangamia, mawazo ya mwanadamu yataweza namna gani kujificha mbele yake? Mwenye mazarau hapendi kuonywa, hatafuti hata kidogo maoni ya wenye hekima. Moyo wa furaha unaangarisha uso, lakini uchungu unavunja moyo. Mwenye akili anatafuta maarifa, lakini wapumbafu wanajikulisha upumbafu. Kwa mwenye kuteswa, kila siku ni mbaya, lakini kwa mwenye raha ni sikukuu. Afazali kuwa na kidogo na kumwogopa Yawe, kuliko kuwa na mali nyingi pamoja na taabu. Afazali kula mboga za majani kwa upendo, kuliko karamu ya nyama nono pamoja na chuki. Mutu wa hasira mbaya anasababisha ugomvi, lakini asiyekuwa mwepesi wa hasira anautuliza. Njia ya muvivu inajaa miiba, lakini njia ya mutu wa usawa ni wazi kama barabara kubwa. Mutoto mwenye hekima anamufurahisha baba yake, lakini mupumbafu anamuzarau mama yake. Upumbafu ni furaha kwa mutu asiyekuwa na akili, lakini mwenye akili anachagua njia inayokuwa sawa. Mipango inaharibika kwa kukosa shauri, lakini kwa washauri wengi, inasimama. Kutoa jibu zuri kunafurahisha; neno linalofaa kwa wakati wake ni jema sana! Njia ya mwenye hekima inaelekea juu kwenye uzima, kusudi aepuke kuingia chini katika kuzimu. Yawe anabomoa makao ya wenye kiburi, lakini analinda mipaka ya makao ya mujane. Mawazo ya mwovu ni chukizo kwa Yawe, lakini maneno mema yanamufurahisha. Anayetamani faida ya unyanganyi anataabisha jamaa yake, lakini anayechukia kituliro ataishi. Moyo wa mwenye haki unafikiri mbele ya kujibu, lakini kinywa cha mwovu kinatapika uovu. Yawe anajiweka mbali na watu waovu, lakini yuko karibu na wenye haki kwa kuwasikiliza. Uso wenye kuangaa unafurahisha moyo. Habari njema inarudishia mwili nguvu. Mutu ambaye anasikiliza maonyo mema ana nafasi yake kati ya wenye hekima. Anayekataa kufundishwa anajizarau mwenyewe, lakini anayekubali maonyo anapata ufahamu. Kumwogopa Yawe ni mafundisho ya hekima; mbele ya kuheshimika inafaa kuwa munyenyekevu. Mwanadamu anapanga mipango yake, lakini neno la mwisho ni la Yawe. Matendo yote ya mutu yanaonekana kwake kuwa sawa lakini Yawe anapima nia ya mutu. Tegemea Yawe katika kazi yako, nayo mipango yako itafanikiwa. Yawe ameumba kila kitu kwa kusudi lake, hata waovu kwa ajili ya siku ya maangamizi. Kila mwenye kiburi ni chukizo kwa Yawe. Hakika mutu wa namna hiyo hatakosa kuazibiwa. Kwa wema na uaminifu mutu anaondoa uovu. Kwa kumwogopa Yawe anaepuka ubaya. Yawe akipendezwa na mwenendo wa mutu, anawageuza hata waadui zake kuwa warafiki. Afazali mali kidogo kwa njia ya haki, kuliko mapato mengi kwa njia isiyofuatana na sheria ya Mungu. Mutu anaweza kufanya mipango yake, lakini Yawe anaongoza hatua zake. Mufalme anaamua kwa maongozi toka kwa Mungu. Anapotoa hukumu hapotoki. Mizani na vipimo vya kweli ni vya Yawe. Mawe yote ya kupimia katika mufuko ni kazi yake. Ni chukizo kubwa kwa wafalme kutenda uovu, maana musingi wa mamlaka yao ni haki. Mufalme anapendelea mutu anayesema maneno ya haki. Anamupenda mutu anayesema kwa usawa. Hasira ya mufalme ni kama mujumbe wa kifo; mutu mwenye hekima ataituliza. Uso wa mufalme ukiangaa, kuna uzima; kupendwa naye ni kama wingu la mvua kwa shamba. Kupata hekima ni bora kuliko zahabu; kupata akili ni chaguo bora kuliko feza. Njia ya watu wa usawa ni kujiepusha na uovu; anayechunga njia yake anachunga maisha yake. Kiburi kinatangulia maangamizi; majivuno yanatangulia maanguko. Afazali kuwa munyenyekevu pamoja na masikini, kuliko kugawanyana vitu vya unyanganyi pamoja na wenye kiburi. Anayefikiri sana juu ya neno atafanikiwa. Heri mutu yule anayemutumainia Yawe. Mwenye hekima ndani ya moyo anaitwa mwenye akili; neno la kupendeza linawavuta watu. Hekima ni chemichemi ya uzima kwa yule anayekuwa nayo, lakini upumbafu ni azabu ya wapumbafu. Moyo wa mwenye hekima unamwezesha kusema kwa hekima; unayafanya maneno yake yakuwe ya kuvutia. Maneno mazuri ni kama asali. Ni matamu kwa nafsi na yenye kuupatia mwili afya. Kuna njia mutu anayoona kuwa sawa, lakini kwa mwisho inaongoza kwenye kifo. Njaa inamusukuma mutu kufanya kazi, maana tamaa ya kinywa chake inamupa bidii. Mutu mwovu anapanga kutenda uovu. Maneno yake ni kama moto mukali. Mutu mupotovu anatawanya ugomvi, na muchonganishi anatenganisha warafiki. Mutesaji mukali anamushawishi jirani yake na kumwongoza katika njia mbaya. Anayekonyeza jicho amepanga kutenda maovu; anayekaza midomo amekwisha kutenda mabaya. Kuwa na imvi za uzee ni taji la utukufu; zinapatikana kwa maisha ya haki. Asiyekuwa mwepesi wa hasira ni bora kuliko mwenye nguvu. Anayetawala nafsi yake ni bora kuliko anayetaka muji. Kura inapigwa kwa kujua yatakayotukia, lakini uamuzi ni wa Yawe. Afazali kula mukate wenye kukauka kwa amani kuliko karamu katika nyumba ya ugomvi. Mutumwa mwenye hekima atatwaa nafasi ya mwana mupumbafu. Atapata sehemu ya urizi wa jamaa hiyo. Zahabu na feza vinapimwa kwa moto, lakini Yawe ndiye anayepima mioyo ya watu. Mutenda maovu anasikiliza maneno mabaya; mwongo anategea sikio ulimi mudanganyifu. Anayechekelea masikini anamutukana Muumba wake; anayefurahia hasara hatakosa kuazibiwa. Taji la sifa la wazee ni wajukuu wao. Heshima ya wana ni baba yao. Maneno mazuri hayastahili katika kinywa cha mupumbafu, zaidi sana maneno ya uongo katika kinywa cha kiongozi! Kwa anayetoa kituliro ni kama hirizi; kila kitu anachofanya yeye anafanikiwa. Anayesamehe makosa anajenga urafiki, lakini anayekumbusha makosa anatenga warafiki. Onyo kwa mwenye akili lina maana, kuliko mapigo mia moja kwa mupumbafu. Nia ya mutu mwovu ni kuasi tu; mujumbe mubaya atatumwa juu yake. Afazali kukutana na dubu dike aliyenyanganywa watoto wake, kuliko kukutana na mupumbafu katika upumbafu wake. Mwenye kulipa mazuri kwa mabaya, mabaya hayataondoka katika nyumba yake. Kuanzisha ugomvi ni kama kufungua maji ya kisima; achana na ugomvi mbele haujafurika. Kumuhesabu mwovu kuwa na haki na kumwazibu asiyekuwa na kosa, yote mawili ni chukizo kwa Yawe. Kwa nini mupumbafu kuwa na feza katika mukono kwa kununua hekima, wakati yeye mwenyewe hana akili? Rafiki wa kweli ni rafiki siku zote. Ndugu anazaliwa kusudi asaidie wakati wa taabu. Mutu asiyekuwa na akili anajitoa rehani kwa deni ya mutu mwingine. Anayependa ugomvi anapenda zambi. Anayejivuna anajitafutia maangamizi. Mwenye moyo mupotovu hafanikiwi, na musema uongo anapatwa na hasara. Mutoto mupumbafu ni huzuni kwa baba yake, na baba wa mupumbafu hana furaha. Moyo wenye furaha ni dawa, lakini moyo wenye huzuni unakondesha mwili. Mutu mubaya anapokea kituliro kwa siri kusudi apate kupotosha haki. Hekima ni mbele ya uso wa mwenye akili, lakini macho ya mupumbafu yanaangalia kwa miisho ya dunia. Mutoto mupumbafu ni huzuni kwa baba yake, na uchungu kwa mama yake muzazi. Si vizuri kumwazibu mutu asiyekuwa na kosa; ni kosa kuwapiga fimbo wenye heshima. Asiyesema sana ana maarifa; mutu mutulivu ni mwenye ufahamu. Hata mupumbafu akinyamaza, anaonekana kuwa na hekima; akifunga kinywa chake anaonekana kuwa mwenye akili. Anayejitenga na wenzake anajipendelea mwenyewe; anakasirika akipewa shauri lolote jema. Mupumbafu hapendezwi na ufahamu; kitu cha maana kwake ni maoni yake tu. Mwovu anapokuja, mazarau yanakuja vilevile; pamoja na haya, matusi yanakuja. Maneno ya kinywa cha mutu ni kilindi cha maji; chemichemi ya hekima ni kijito kinachobubujika. Si vizuri kumupendelea mutu mwovu, na kumunyima sheria mutu wa haki. Maneno ya mupumbafu yanaleta ugomvi; kila neno analosema linasababisha azabu. Kinywa cha mupumbafu kinamwangamiza mwenyewe; mudomo wake ni mutego wa kumunasa yeye mwenyewe. Maneno ya muchongeaji ni kama chakula kitamu ambacho kinashuka mpaka ndani kabisa ya tumbo. Mutu muvivu katika kazi yake ni ndugu ya muharibifu. Jina la Yawe ni munara imara; mwenye haki anaukimbilia na kuwa salama. Tajiri anazani kwamba mali ni makimbilio yake; anafikiri hayo ni ukuta murefu unaomulinda. Majivuno ya ndani ya moyo yanaleta maangamizi, lakini unyenyekevu unaleta heshima. Kujibu mbele ya kusikiliza ni upumbafu na jambo la haya. Roho ya mutu inaweza kuvumilia ugonjwa, lakini ukiwa umevunjika moyo, utavumilia namna gani? Mutu mwenye akili anajipatia maarifa; sikio la mwenye hekima linatafuta maarifa. Zawadi inamufungulia mutu milango; inaweza kumufikisha mutu mbele ya mukubwa. Anayejitetea wa kwanza anaonekana kuwa na haki, mpaka pale mupinzani wake atakapoanza kumupinga. Kura inakomesha ubishi; inaamua kati ya wakubwa wanaopingana. Ndugu aliyetendewa kosa ni mugumu kuliko muji wenye ukuta; magomvi yanakaza kama vile vifungio vya mulango wa ukuta. Maneno ya mutu yanaweza kumushibisha; anatosheka kwa matokeo ya maneno yake. Ulimi una nguvu ya kuleta uzima na kuua; wanaopenda kuutumia watakula matunda yake. Anayemupata muke amepata kizuri; ni zawadi kutoka kwa Yawe. Masikini anaomba kwa unyenyekevu, lakini tajiri anajibu kwa ukali. Warafiki wengi wanaweza kumwangusha mutu, lakini kuna rafiki mwaminifu kuliko ndugu. Afazali masikini mwenye mwenendo mukamilifu kuliko mutu mupotovu wa maneno na mupumbafu. Haifai mutu kuwa bila akili; mwenda harakaharaka anajikwaa. Mutu akijiangamiza kwa upumbafu wake, anaielekeza hasira yake kwa Yawe. Mali inavuta warafiki wengi wapya, lakini masikini anaachwa na rafiki yake. Mushuhuda mwongo hatakosa kuazibiwa; anayesema uongo hataepuka azabu. Watu wengi wanajipendekeza kwa wakubwa; kila mutu anataka kuwa rafiki wa mutu mwenye kupana. Masikini anachukiwa na wandugu zake; warafiki zake ndio zaidi: wanamukimbia! Hata awabembeleze namna gani, hatawapata. Anayejipatia hekima anapenda nafsi yake; anayeshika ufahamu atastawi. Mushuhuda mwongo hatakosa kuazibiwa; anayesema uongo ataangamia. Haifai kwa mupumbafu kuishi kwa raha; tena ni vibaya zaidi mutumwa kuwatawala wakubwa. Mwenye akili hakasiriki upesi; kusamehe makosa ni utukufu kwake. Kasirani ya mufalme ni kama ngurumo ya simba, lakini upendo wake ni kama umande juu ya majani. Mutoto mupumbafu ni hasara kwa baba yake; na ugomvi wa muke ni kama matone ya mvua yasiyoisha. Nyumba na mali ni urizi mutu anaopata kwa babu zake, lakini muke mwenye akili anatoka kwa Yawe. Uvivu ni kama usingizi muzito; mutu muvivu atateseka kwa njaa. Anayeshika amri analinda maisha yake; anayezarau agizo atakufa. Anayemusaidia masikini anamukopesha Yawe; Yawe atamulipa kwa tendo lake jema. Azibu mwana wako wakati kungali bado tumaini lakini usitafute kumwangamiza. Mutu wa hasira kali anapaswa kupata azabu; ukimwachilia mara moja itakuomba kumwachilia tena. Sikiliza shauri na kupokea mafundisho, upate hekima ya kukufaa kwa siku zinazokuja. Katika moyo wa mutu muna mipango mingi, lakini anachokusudia Yawe ndicho kitakachokamilika. Kitu kinachotakiwa kwa mutu ni uaminifu; afazali mutu masikini kuliko mutu mwongo. Kumwogopa Yawe kunaongoza kwenye uzima; anayemwogopa anajaliwa pumziko la kutoshelea, wala hatapatwa na ubaya wowote. Muvivu anatia mukono wake katika sahani lakini hauinui mpaka kwenye midomo. Umwazibu mwenye kuzarau naye mujinga atapata akili; umwonye mwenye akili naye atapata maarifa. Anayemutesa baba yake na kumufukuza mama yake ni mutoto asiyefaa na mupotovu. Mwana wangu, ukiacha kusikiliza mafundisho, mara moja utapotea mbali na maneno ya maarifa. Mushuhuda asiyefaa kitu anazarau sheria ya Mungu; na kinywa cha mwovu kinameza uovu. Azabu iko tayari kwa wenye kuzarau, na mapigo kwa migongo ya wapumbafu. Divai inaleta mazarau na kileo kinaleta ugomvi; yeyote anayevutwa navyo hana hekima. Kasirani kali ya mufalme ni kama simba anayenguruma; anayemukasirikisha anahatarisha maisha yake. Ni jambo la heshima kuepuka ugomvi; wapumbafu ndio wanaogombana. Muvivu halimi wakati wa kulima; wakati wa mavuno atatafuta lakini hatapata kitu. Mafikiri ya mutu ndani ya moyo wake ni kama kilindi cha maji; lakini mutu mwenye akili anajua kuyachota mule. Watu wengi wanajivunia kuwa wema, lakini mwaminifu wa kweli anapatikana wapi? Heri watoto wa mutu wa haki mwenye mwenendo mukamilifu! Mufalme anapoikaa kwa kutoa hukumu, anapepeta uovu wote kwa macho yake. Nani anayesubutu kusema: “Nimetakasa moyo wangu; mimi nimetakasika na zambi yangu?” Mizani danganyifu na vipimo danganyifu, vyote ni chukizo kwa Yawe. Hata mutoto anajulikana kwa matendo yake, kama ni safi na sawa. Sikio linalosikia na jicho linaloona, vyote viwili vimefanywa na Yawe. Usipende usingizi usikuje kuwa masikini; ukuwe macho nawe utakuwa na chakula kingi. Mununuzi analalamika: “Hakifai, hakifai,” lakini akiondoka anajisifu amepunguziwa bei. Kuna zahabu na wingi wa mawe ya bei kali; lakini kitu cha bei kali zaidi ni maneno ya maarifa! Mutu akiahidi kumukopesha mutu asiyejulikana, unyanganye nguo yake kuwa rehani. Chakula kinachopatikana kwa udanganyifu ni kitamu, lakini nyuma kinakuwa kama muchanga ndani ya kinywa. Mipango mizuri inafanyika kwa kushauriana; ukitaka kuanza vita inafaa kufikiri kwanza. Mupiga domo hafichi siri. Kwa hiyo umwepuke mutu wa kusemasema. Anayemulaani baba yake au mama yake, mwangaza wa uzima wake utazimika kama taa katika giza. Mali iliyopatikana kwa haraka kwa mwanzo, haitakuwa ya heri kwa mwisho. Usiseme: “Nitalipiza ubaya niliotendewa.” Umutegemee Yawe naye atakusaidia. Mizani danganyifu ni chukizo kwa Yawe, na vipimo visivyokuwa vya haki ni kitu kibaya. Hatua za mutu zinaongozwa na Yawe; mwanadamu anaweza namna gani kuelewa njia yake? Ni hatari kusema kwa muzaha “Nitamutolea Mungu hiki!” na kuanza kufikiri nyuma ya kufanya naziri ile. Mufalme mwenye hekima anapepeta waovu; anawaazibu bila huruma. Zamiri ya mutu ni taa ya Yawe; inachunguza nafsi ya mutu mpaka ndani kabisa. Wema na uaminifu unamukinga mufalme; utawala wake unaimarishwa kwa haki. Utukufu wa vijana ni nguvu zao. Uzuri wa wazee ni kichwa chenye imvi. Mapigo yanayoumiza ni dawa ya kuondoa uovu; fimbo inasafisha nafsi mpaka ndani kabisa. Moyo wa mufalme ni kama maji yanayotiririka; Yawe anauongoza popote anapopenda. Matendo yote ya mutu ni sawa katika macho yake, lakini Yawe anapima mioyo. Kutenda mambo ya haki na kufuata sheria ya Mungu kunamupendeza Yawe kuliko sadaka. Macho ya kiburi na moyo wa majivuno vinaonyesha wazi zambi ya waovu. Mipango ya mutu wa bidii inaleta mali kwa wingi, lakini kila mutu anayetenda kwa harakaharaka anapata umasikini. Mali inayopatikana kwa udanganyifu ni muvuke unaopita na mutego wa kifo. Ukali wa waovu utawaangamiza, maana wanakataa kutenda mambo ya haki. Njia ya mutu mwenye kosa imepotoka, lakini mwenendo wa mwenye moyo safi ni sawa. Afazali kuishi pembeni juu ya paa, kuliko kuishi ndani ya nyumba pamoja na mwanamuke mugomvi. Mutu mwovu anatamani kutenda uovu; hata kwa jirani yake hana huruma. Mwenye kiburi anapoazibiwa, mujinga anapata hekima. Ukimufundisha mwenye hekima, unamupatia maarifa. Mwenye haki anajua yanayokuwa katika nyumba ya waovu: waovu wanaangushwa chini na kuangamia. Anayekataa kusikia kilio cha masikini hatasikilizwa atakapolilia musaada. Hasira inatulizwa kwa zawadi ya siri; kituliro kinachotolewa kwa uficho kinatuliza kasirani. Haki ya sheria ikifuatwa, watu wema wanafurahi lakini watu waovu wanafazaika. Anayetangatanga mbali na njia ya ufahamu, atajikuta ametua kati ya wafu. Anayependa raha atakuwa masikini; anayefikiria tu kula na kunywa hatatajirika. Mwovu atakuwa malipo kwa ukombozi wa wenye haki; nao wasiokuwa waaminifu kwa pahali pa watu wa usawa. Afazali kuishi katika jangwa kuliko kukaa na mwanamuke mugomvi na muchokozi. Katika nyumba ya mwenye hekima kuna hazina za bei kali, lakini mupumbafu anaponda mali yake yote. Anayetafuta haki na wema atapata uzima, haki, na heshima. Mwenye hekima anaweza kuteka muji wa wenye nguvu na kukiporomosha kikingio wanachokitegemea. Anayechunga kinywa chake na ulimi wake, anajiepusha na matatizo. Mwenye kiburi na majivuno jina lake ni “Mazarau”; anatenda kwa kujivuna tu. Muvivu anakufa kwa kutokutimizwa kwa tamaa zake, maana mikono yake haitaki kufanya kazi. Muchana kutwa mwovu anatamani kupata kitu, lakini mwenye haki anatoa, tena bila mipaka. Sadaka ya mwovu ni kitu cha kuchukiza sana. Inachukiza zaidi akiitoa kwa nia mbaya. Mushuhuda mwongo ataangamia, lakini anayejua kusikiliza hawezi kunyamazishwa. Mutu mwovu anajionyesha kuwa hodari, lakini mutu wa usawa anafikiri vizuri juu ya mwenendo wake. Hakuna hekima, ufahamu, wala shauri yoyote ya mutu, itakayoweza kupingana na Yawe. Farasi anatayarishwa kwa vita, lakini ushindi unaletwa na Yawe. Afazali kuwa na sifa nzuri kuliko mali mengi. Kupata kukubaliwa ni bora kuliko feza au zahabu. Watajiri na wamasikini wana hali hii moja: Yawe ni Muumba wao wote. Mwenye akili anaona hatari na kujificha, lakini wajinga wanajitokeza mbele na kuumia. Ukinyenyekea na kumwogopa Yawe, utapata zawadi ya fanaka, heshima, na uzima. Njia ya waovu imejaa miiba na mitego; anayetaka kulinda maisha yake ataiepuka. Umufundishe mutoto njia anayopaswa kufuata, naye hataiacha hata katika uzee. Tajiri anamutawala masikini. Mwenye kukopesha ni mutumwa wa mwenye kukopeshwa. Anayepanda ubaya atavuna hasara. Uwezo wake wa kutenda mabaya utavunjwa. Mutu mwenye kuwa tayari kusaidia atabarikiwa, maana anagawanya chakula chake na masikini. Umufukuze mwenye kiburi na fujo itatoweka, na ugomvi na matusi vitakoma. Mwenye nia safi na maneno mazuri atakuwa rafiki wa mufalme. Yawe analinda maarifa lakini anayavuruga maneno ya waovu. Muvivu anasema: “Kuna simba inje. Nitauawa katika njia.” Kinywa cha mwasherati ni shimo refu; anayechukiwa na Yawe atatumbukia ndani yake. Ujinga umefungwa ndani ya moyo wa mutoto, lakini fimbo ya kufundisha itaufukuza mbali. Anayemutesa masikini kwa kujitajirisha na anayewapa watajiri zawadi, wote wawili wataishia kuwa wamasikini. Tega sikio usikie maneno ya wenye hekima; elekeza moyo wako kwa maarifa yangu. Wewe utafurahi kama utayaweka ndani ya moyo, na kuyarudiliarudilia kila wakati. Ninayependa kumufundisha leo ni wewe, kusudi tumaini lako likuwe kwa Yawe. Nimekuandikia misemo makumi tatu, misemo ya maonyo na maarifa, kwa kukufundisha mambo yanayokuwa sawa na kweli; na mutu akikuuliza upate kumupa jibu la kweli. Usinyanganye masikini mali yake kwa sababu ni masikini, wala usimunyime mukosefu haki yake katika tribinali. Maana Yawe atawatetea; atagandamiza maisha ya wale wanaowagandamiza. Usifanye urafiki na mutu wa hasira, wala usiandamane na mwenye kukasirika upesi. Usijifunze mwenendo wake, na kujinasa kabisa katika mutego. Usikuwe mumoja wa wale ambao wanajitoa rehani kwa madeni ya wengine. Ikiwa hauna chochote cha kulipa, hata kitanda unacholalia kitanyanganywa! Usiondoe kitambulisho cha mupaka wa zamani, ambacho kiliwekwa na babu zako. Kuna mutu mwenye akili na maarifa ndani ya kazi? Yule atawatumikia wafalme; hatawatumikia watu wasiofaa. Ukikaa kwa kula pamoja na mutawala, usisahau hata kidogo uko pamoja na nani. Zuia sana hamu yako, ikiwa wewe unapenda sana kula. Usitamani vyakula vyake vizuri, maana vinaweza kukudanganya. Usijichokeshe na kutafuta utajiri; acha kufikiri juu yake. Macho yako yatakapokuwa yanaanza tu kuuona, nao utatoweka mara moja. Maana hakika utajiri unaota mabawa, unaruka na kutoweka katika anga kama tai. Usikule chakula cha mutu muchoyo, wala usitamani vyakula vyake vizurivizuri, maana ndani ya moyo wake anahesabu unachokula. Atakuambia: “Kula, kunywa!” Lakini ndani ya moyo wake hayuko pamoja nawe. Utatapika vipande ulivyokula; shukrani zako zote zitakuwa za bure. Usiseme maneno yako mbele ya mupumbafu, maana atazarau hekima ya maneno yako. Usiondoe kitambulisho cha mupaka wa zamani, wala usinyanganye mashamba ya wayatima, maana Mungu, Mukombozi wao, ni mwenye nguvu, naye atatetea haki yao nawe utaonekana kuwa na kosa. Tumia akili yako kwa kufuata mafundisho; tumia masikio yako kwa kusikiliza maarifa. Usiache kufundisha mutoto; ukimupiga fimbo hatakufa. Ukimupiga fimbo, utayaokoa maisha yake na kuzimu. Mwana wangu, moyo wako ukiwa wenye hekima, moyo wangu vilevile utakuwa wenye furaha. Moyo wangu utashangilia, midomo yako itakaposema maneno ya usawa. Moyo wako usiwaonee wivu wenye zambi, lakini endelea kumwogopa Yawe siku zote. Hakika siku nzuri zitafika na tumaini lako halitakuwa la bure. Sikia, mwana wangu, ukuwe na hekima; fikiri sana jinsi unavyoishi. Usikuwe mumoja kati ya walevi wa divai, wala walafi wenye kupenda nyama, maana walevi na walafi wataishia kuwa wamasikini. Usingizi utawavalisha nguo za kupasukapasuka. Umusikilize baba yako aliyekuzaa, wala usimuzarau mama yako akizeeka. Nunua ukweli, wala usiuuzishe; nunua hekima, mafundisho na akili. Baba wa mutoto mwenye haki atajaa furaha; anayezaa mutoto mwenye hekima atamufurahia. Uwafurahishe baba na mama yako; mama yako aliyekuzaa afurahi. Mwana wangu, unisikilize kwa uangalifu, ufuate mwenendo wa maisha yangu. Kahaba ni kama shimo refu; mwanamuke mugeni ni kama kisima chembamba. Yeye anavizia kama munyanganyi, anasababisha wanaume wengi kukosa uaminifu. Ni nani wenye taabu? Ni nani wenye huzuni? Ni nani wenye ugomvi? Ni nani wenye malalamiko? Ni nani wenye vidonda bila sababu? Ni nani wenye macho mekundu? Ni wale ambao hawabanduki penye divai, wale ambao wanatafuta divai iliyochanganywa. Usiitamani divai hata kwa wekundu wake, hata kama inametameta katika kilauri, na kushuka vizuri unapoikunywa. Kwa mwisho inauma kama nyoka; inachoma kama fira mwenye sumu. Macho yako yataona mambo ya ajabu, moyo wako utatoa mambo yaliyopotoka. Utakuwa kama mutu anayelala katikati ya bahari, kama mutu anayelala juu ya mulingoti wa mashua. Utasema: “Nimepigwa, lakini sikuumia; wamenipondaponda, lakini sikusikia kitu. Nitaamuka saa gani kusudi nitafute kinywaji kingine?” Usiwaonee wivu watu waovu, wala usitamani kuwa pamoja nao, maana mafikiri yao yote ni juu ya kutesa tu, nayo midomo yao inasema mabaya. Nyumba inajengwa kwa hekima, na kuimarishwa kwa ufahamu. Kwa maarifa vyumba vyake vinajazwa vitu vya bei kali na vya kupendeza. Kuwa na hekima na maarifa ni bora kuliko kuwa na nguvu. Maana kwa mipango mizuri unaweza kupigana vita, na kwa washauri wengi ushindi unapatikana. Kwa mupumbafu hekima ni ngumu kuielewa; penye mukutano wa mashauri hafungui mudomo. Anayefikiria kutenda maovu siku zote, ataitwa mutu mwenye fitina. Mupango mupambafu anaofikiri ni zambi; mwenye kuzarau anachukiwa na kila mutu. Ukiregea wakati wa shida, basi wewe ni muzaifu kweli. Umwokoe mutu anayepelekwa kuuawa kwa bure; usisite kumwopoa anayeuawa bila kosa. Usiseme kisha: “Hatukujua!” Maana Mungu anayepima mioyo ya watu anaona; yeye atakulipa kulingana na matendo yako! Mwana wangu, ukule asali maana ni nzuri; sega la asali ni tamu katika kinywa chako. Ndivyo hekima itakavyokuwa katika nafsi yako; ukiipata, siku nzuri zitakuja na tumaini lako halitakuwa la bure. Usivizie kama mwovu kwa kushambulia makao ya mutu wa haki, wala usijaribu kuharibu nyumba yake, maana mutu wa haki anaanguka mara nyingi naye anainuka tena, lakini mutu mwovu anaangamizwa na hasara. Usishangilie kuanguka kwa adui yako; usifurahie ndani ya moyo wako kujikwaa kwake, maana Yawe akiona yale hatapendezwa; ataacha kumuazibu. Usihangaike kwa sababu ya watenda mabaya, wala usiwaonee wivu watu waovu, maana siku mbaya zitamufikia mwovu; taa ya uzima wake itazimika. Mwana wangu, uwaheshimu Yawe na mufalme, wala usishirikiane na waasi, maana maangamizi yatawatokea kwa rafla. Hakuna anayejua magumu watakayoleta. Hii ni misemo mingine ya wenye hekima. Kupendelea watu katika hukumu si vizuri. Anayemwachilia mutu mwenye kosa analaaniwa na watu na kuchukiwa na mataifa. Lakini wanaowaazibu waovu watapata furaha, na baraka nzuri zitawafikia. Jibu linalokuwa la haki ni kama busu la rafiki. Kwanza fanya kazi zako inje na kutayarisha kila kitu katika shamba. Kisha jenga nyumba yako. Usishuhudie bure juu ya jirani yako, wala usiseme uongo juu yake. Usiseme: “Nitamutendea kama vile alivyonitendea! Inapasa kulipiza kisasi!” Nilipitia karibu na shamba la muvivu, ni kusema shamba la mizabibu la mutu mupumbafu, niliona kwamba lilikuwa limeota miiba, majani yalikuwa yamefunika eneo lake lote, na ukuta wake wa mawe ulikuwa umebomoka. Niliangalia, nikawaza. Kwa mwisho nikapata fundisho: Lala tu kidogo, sinzia tu kidogo, kunja mikono yako tu upumzike, lakini kumbuka kwamba unapokuwa katika usingizi, umasikini utakufikia kama munyanganyi, ukosefu kama mutu mwenye silaha. Hizi nazo ni mezali nyingine za mufalme Solomono zilizoandikwa na watu wa Hezekia, mufalme wa Yuda. Mungu anatukuzwa kwa kuficha mambo, lakini wafalme wanatukuzwa kwa kuchunguza mambo. Kama vile mbingu zinavyokuwa mbali juu na dunia mbali chini, ndivyo inavyokuwa vigumu kuelewa akili za mufalme. Toa takataka katika feza, na mufuaji wa vyuma atakutengenezea chombo kizuri. Uwaondoe waovu mbele ya mufalme, na utawala wake utaimarika katika haki. Usijipendekeze kwa mufalme, wala usijifanye mutu mukubwa, maana ni heri kuambiwa: “Kuja huku mbele”, kuliko kuporomoshwa mbele ya mukubwa. Mambo uliyoona kwa macho yako, usiharakishe kuyapeleka katika tribinali; maana utafanya nini kwa mwisho, kama jirani yako anakupatisha haya? Utengeneze ugomvi na mwenzako peke yake, na kila mumoja wenu asitoe siri ya mwenzake; watu wanaokusikia wasikuzarau, nawe usijiharibishie heshima kwa siku zote. Neno linalosemwa kwa wakati unaofaa, ni kama michoro ya zahabu juu ya feza. Onyo la mwenye hekima kwa mutu musikilivu ni bora kuliko pete au ushanga wa zahabu safi. Mujumbe mwaminifu anamufurahia yule aliyemutuma, kama maji ya baridi wakati wa joto la mavuno. Kama vile mawingu na upepo bila mvua, ndivyo anavyokuwa mutu anayeahidi zawadi na haitoi. Kwa uvumilivu mutawala anaweza kusadikishwa; ulimi laini unavunja mifupa. Unapopata asali, kula sehemu ya kukutoshelea, kusudi usishibe na kuitapika. Usimutembelee jirani yako mara kwa mara, kusudi asichoke nawe na kukuchukia. Mutu anayetoa ushuhuda wa uongo juu ya mwenzake, ni hatari kama nyundo, upanga au mushale mukali. Kumutegemea mutu asiyeaminiwa wakati wa taabu, ni kama kutegemea jino zaifu au muguu ulioteguka. Kumwimbia mutu mwenye huzuni ni kama kumuvua nguo wakati wa baridi, au kutia siki katika kidonda. Adui yako akiwa na njaa, umupe chakula; akiwa na kiu, umupe maji ya kunywa. Hivyo utamufezehesha, kama vile kumwanga makaa ya moto juu ya kichwa chake. Yawe atakupa zawadi. Upepo wa kaskazini unaleta mvua; vilevile mwenye kusingiziana analeta chuki. Afazali kuishi pembeni juu ya paa, kuliko kuishi ndani ya nyumba pamoja na mwanamuke mugomvi. Kama vile maji baridi kwa mwenye kiu, ndivyo habari njema kutoka mbali inavyokuwa. Mwenye haki anayekubali kufuata mambo ya mwovu ni chemichemi iliyochafuliwa au kisima kinachotofuliwa. Si vizuri kula asali nyingi sana; vilevile haifai kujipendekeza sana. Mutu asiyeweza kuzuia hasira yake ni kama muji usiokuwa na ulinzi unaposhambuliwa. Heshima anayopewa mupumbafu haifai. Ni kama teluji ya wakati wa kipwa, au mvua ya wakati wa mavuno. Kama vile ndege anavyorukaruka, vilevile laana isiyokuwa na sababu haimupati mutu. Kiboko ni kwa farasi, lijamu ni kwa punda, na fimbo ni kwa mugongo wa mupumbafu. Usimujibu mupumbafu kipumbafu, kusudi usifanane naye. Umujibu mupumbafu kama kufuatana na upumbafu wake, kusudi asijione kuwa mwenye hekima zaidi. Kutuma ujumbe kwa mukono wa mupumbafu ni kama kujikata miguu au kujitafutia mateso. Mezali katika midomo ya mupumbafu ni kama miguu ya kiwete inayoninginia. Kumupa mupumbafu heshima ni kama kufunga jiwe kwenye mujeledi. Mezali katika kinywa cha mupumbafu ni kama tawi lenye miiba katika mukono wa mulevi. Mutu anayemulipa mupumbafu au mulevi kusudi amutumikie, ni kama mupiga upinde anayeumiza kila mutu. Mupumbafu anayerudiliarudilia upumbafu wake ni kama imbwa anayekula matapiko yake. Unamwona mutu anayejiona kuwa mwenye hekima? Afazali kumutumainia mupumbafu kuliko yule. Muvivu anasema: “Kuna simba kali inje. Kuna simba katika njia.” Kama vile mulango unavyozunguka kwenye vyuma vya kuukamatia, ndivyo muvivu anavyogeuka juu ya kitanda chake. Muvivu anatia mukono wake katika sahani, lakini anachoka kwa kuuinua mpaka kwenye mudomo. Muvivu anajiona kuwa mwenye hekima kuliko watu saba wanaoweza kujibu kwa akili. Anayejiingiza katika ugomvi usiomwelekea, ni kama mutu anayeshika masikio ya imbwa anayepita. Kama vile mwenda-wazimu anavyotupa mienge ya moto, mishale, na kifo, ndivyo mutu ambaye anadanganya jirani, kisha anasema: “Nilikuwa ninafanya muzaha tu!” Bila kuni, moto unazimika; bila mwenye kuchochea, ugomvi unamalizika. Kama vile makaa au kuni vinachochea moto, ndivyo mugomvi anachochea ugomvi. Maneno ya muchongeaji ni kama chakula kitamu; yanashuka mpaka ndani kabisa ya tumbo. Kama vile rangi yenye kungaa iliyopakwa juu ya chungu cha udongo, ndivyo maneno matamu yenye nia mbaya yanavyokuwa. Mwenye chuki anaficha chuki yake kwa maneno mazuri, lakini uovu unajaa ndani ya moyo wake. Akisema maneno mazuri usimwaminie. Ndani ya moyo wake kuna machukizo mengi. Anaweza kuficha chuki yake, lakini nia zake mbaya zitajulikana kwa wote. Anayechimbia mwenzake shimo, anatumbukia ndani mwenyewe; anayewaporomoshea wengine jiwe, litamurudilia mwenyewe. Anayesema uongo anachukia wale anaowaumiza, naye anayebembeleza analeta maangamizi. Usijisifie kwa ajili ya kesho. Haujui siku ya leo itakuletea nini. Acha watu wengine wakusifu, kuliko kujisifu kwa mudomo wako wewe mwenyewe. Jiwe ni zito na muchanga vilevile, lakini uchokozi wa mupumbafu ni muzito zaidi. Kasirani ni kali na hasira inaangamiza; lakini ni nani anayeweza kupingana na wivu? Afazali mutu anayekuonya waziwazi, kuliko yule anayeficha upendo. Makaripio ya rafiki yanaonyesha uaminifu, lakini busu la adui ni udanganyifu. Aliyeshiba anakataa hata asali, lakini kwa mwenye njaa kila chakula kichungu ni kitamu. Mutu aliyepotea mbali na kwake ni kama ndege aliyepotea mbali na chicha yake. Mafuta na marasi vinafurahisha moyo, vilevile utamu wa urafiki kuliko kujitoshelea mwenyewe. Usisahau warafiki zako wala wa baba yako. Ukipatwa na magumu usikimbilie kwa ndugu yako. Afazali jirani ambaye iko karibu kuliko ndugu anayekuwa mbali. Ukuwe na hekima, mwana wangu, upate kunifurahisha moyo, nami sitakosa neno la kumujibu mutu yeyote anayenizarau. Mwenye akili anaona hatari na kujificha, lakini wajinga wanajitokeza mbele na kuumia. Mutu akiahidi mbele yako kubeba muzigo wa mutu mwingine, unyanganye nguo yake; utwae rehani kwake maana amebeba muzigo wa mutu mwingine. Anayemusalimia jirani yake kwa kelele asubui mapema, itahesabiwa kwamba amemutakia laana. Muke mugomvi ni kama matone ya mvua yasiyoisha siku ya mvua. Kumuzuia ni sawa na kuzuia upepo, au kukamata mafuta kwa mukono. Chuma kinanoa chuma, vilevile mutu anafundishwa na mwenzake. Anayetunza muti wa tini atakula matunda yake. Anayetumikia bwana wake ataheshimiwa. Kama uso unavyojiona wenyewe katika maji, ndivyo mutu anavyojijua mwenyewe ndani ya moyo. Kuzimu na shimo la kuangamia havishibi hata kidogo, vilevile macho ya watu hayashibi. Zahabu na feza vinapimwa kwa moto, na mutu anapimwa kutokana na sifa zake. Hata kama ukitwanga mupumbafu katika kinu, sawa na ngano, hautaweza kumutenganisha na upumbafu wake. Angalia vizuri hali ya makundi yako ya nyama; tunza vizuri nyama wako. Maana utajiri haudumu milele, wala taji haidumu kwa vizazi vyote. Nyuma ya kukata majani, wakati nyasi zinachipuka upya, kusanya majani toka kwenye milima. Kondoo watakupatia sufu kwa ajili ya nguo zako, mbuzi nao utawauzisha na kujinunulia mashamba; watakupa maziwa ya kukutoshelea na jamaa yako, na kwa ajili ya wajakazi wako. Waovu wanakimbia ijapokuwa hawafukuzwi na mutu, lakini wenye haki ni hodari kama simba. Taifa lenye fujo lina viongozi wengi, lakini kwa kiongozi mumoja mwenye akili na maarifa kuna utengemano. Mutu mwenye hitaji anayewatesa wamasikini, anafanana na mvua kubwa inayoharibu mimea. Watu wanaovunja sheria wanasifu waovu, lakini wanaoshika sheria wanapingana nao. Waovu hawaelewi haki ya sheria, lakini wanaomwogopa Yawe wanaielewa kabisa. Afazali masikini mwenye mwenendo mukamilifu, kuliko tajiri anayeishi kwa upotovu. Mutoto anayeshika sheria ni mwenye hekima, lakini rafiki wa walafi anafezehesha baba yake. Anayeongeza mali yake kwa mazidio na kulipisha faida, anamukusanyia mwingine mwenye kuwahurumia wamasikini. Anayekataa kuisikia sheria, yule, hata maombi yake, ni chukizo kwa Mungu. Anayepotosha mutu wa usawa katika njia mbaya, ataanguka katika shimo lake mwenyewe. Wakamilifu watarizi mazuri. Tajiri anajiona mwenyewe kuwa mwenye hekima, lakini masikini mwenye akili atamufichua. Watu wa haki wakipata madaraka, kuna utukufu mukubwa. Lakini waovu wakitawala, watu wanajificha. Anayeficha makosa yake hatafanikiwa, lakini anayeungama na kuyaacha atahurumiwa. Heri mutu anayemwogopa Yawe siku zote, lakini mwenye moyo mugumu atapata hasara. Mutawala mwovu anayetawala wamasikini ni kama simba anayenguruma au dubu anayeshambulia. Mutawala asiyekuwa na akili anawagandamiza sana watu, lakini anayechukia mali ya udanganyifu atatawala kwa muda murefu. Mutu anayelemewa na kosa ya kuua mutu, atakuwa mukimbizi mpaka katika kaburi. Mutu yeyote asijaribu kumusaidia. Mwenye mwenendo mukamilifu ataponyeshwa, lakini munafiki wa njia mbili ataanguka mara moja. Anayelima shamba lake atapata chakula kingi, lakini anayefuata mambo yasiyofaa atapata umasikini tele. Mutu mwaminifu atapata baraka tele, lakini mwenye pupa ya kuwa tajiri hataepuka azabu. Si vizuri kumubagua mutu. Watu wanafanya mabaya hata kwa ajili ya mukate. Mutu muchoyo anakimbilia mali, wala hajui kwamba ukosefu utamufikia. Anayemwonya mwenzake kwa mwisho atasifiwa naye, kuliko yule anayemubembeleza kwa maneno matamu. Anayeiba mali ya baba yake au ya mama yake na kusema si kosa, anatumika pamoja na yule anayeangamia. Muchoyo anachochea magomvi, lakini anayetegemea Yawe atafanikiwa. Anayetegemea akili yake mwenyewe ni mupumbafu; lakini anayeishi kwa hekima atakuwa salama. Anayesaidia wamasikini hatakosewa kitu, lakini anayekataa kuwaangalia atalaaniwa kwa wingi. Waovu wakitawala, watu wanajificha. Lakini wakiangamia, wenye haki wanaongezeka. Anayeonywa mara nyingi na kuwa mugumu, ataangamia kwa rafla wala hatapata kupona. Wenye haki wakiongozeka, watu wanafurahi. Lakini waovu wakitawala, watu wanalalamika. Anayependa hekima anamufurahisha baba yake; lakini anayeandamana na kahaba anapoteza mali yake. Mufalme akifuata sheria ya Mungu, anaimarisha inchi. Lakini akipenda kituliro, taifa linaangamia. Mwenye kumubembeleza jirani yake, anatega mutego wa kujinasa mwenyewe. Mutu mubaya ananaswa kwa kosa lake, lakini mutu wa haki anaimba na kufurahi. Mwenye haki anajua haki za wamasikini, lakini mutu mwovu hajui mambo hayo. Wenye mazarau wanaleta mavurugo katika muji muzima, lakini wenye hekima wanatuliza kasirani. Mwenye hekima akibishana na mupumbafu, akasirike au acheke, ni mamoja; hatatulia. Wanaopenda kumwanga damu wanachukia mutu mukamilifu, lakini watu wa usawa wanalinda maisha yake. Mupumbafu anaonyesha hasira yake wazi, lakini mwenye hekima anaizuia na kuituliza. Mutawala akisikiliza mambo ya uongo, wakubwa wake wote watakuwa waovu. Masikini na mugandamizaji wanafanana kwa kitu kimoja: wote wawili wamepewa macho na Yawe. Mufalme anayewaamua wamasikini kwa haki, ataona utawala wake unaimarika milele. Azabu na maonyo vinaleta hekima, lakini mutoto aliyeachiliwa anapatisha mama yake haya. Waovu wakiongozeka, zambi zinaongezeka. Lakini wenye haki watashuhudia kuanguka kwao. Umwazibu mwana wako naye hatakupa wasiwasi; yeye atafurahisha moyo wako. Pasipo maono ya kinabii, watu wanashindwa kujizuiza. Heri mutu yule anayeshika sheria. Mutumwa haonyeki kwa maneno matupu; maana ingawa anayaelewa, yeye hatayatii. Unamwona mutu anayesema bila kufikiri? Mutu mupumbafu ni afazali kuliko yeye. Anayebembeleza mutumwa wake tangu utoto, kwa mwisho mutumwa yule atamurizi. Mwenye kasirani anachochea ugomvi, mutu wa hasira anasababisha makosa mengi. Kiburi cha mutu kinamuzaraulisha mwenyewe, lakini munyenyekevu wa roho atapata heshima. Anayeshirikiana na mwizi anajizuru mwenyewe; anasikia laana ikitolewa bila kusema neno. Kuogopa watu ni kujitega mwenyewe, lakini anayemutumainia Yawe yuko salama. Wengi wanapenda kujipendekeza kwa mutawala, lakini mutu anapata haki yake kwa Yawe. Mwovu ni chukizo kwa mwenye haki, naye mwenye haki ni chukizo kwa mwovu. Maneno ya Aguri mwana wa Yake. Maneno ambayo mutu huyu alimwambia Itieli na Ukali. Mimi ni mupumbafu sana, wala si mutu; sina akili ya mwanadamu. Sijajifunza hekima, wala sijui kitu juu ya Mungu Mutakatifu. Ni nani aliyepanda juu mbinguni na kushuka chini? Ni nani aliyekamata upepo katika mukono? Ni nani aliyefunga maji katika kitambaa? Ni nani aliyeweka mipaka yote ya dunia? Jina lake ni nani? Na ni nani jina la mwana wake? Uniambie kama unajua! Maneno yote ya Mungu ni ya kuaminiwa. Yeye ni ngao yao wote wanaomukimbilia. Usiongeze neno katika maneno yake, kusudi asikukaripie, nawe usionekane kuwa mwongo. Ee Mungu, ninakuomba mambo haya mawili, wala usikatae kunitimizia nayo mbele ya kufa kwangu: Uniondolee uongo na udanganyifu; usinipe umasikini wala utajiri; unipatie chakula ninachohitaji, maana nikipata mali mengi nitakusahau; nikisema: “Yawe ni nani?” Au nikiwa masikini nitaiba, na kuzaraulisha jina lako ee Mungu wangu. Usimuchongee mutumwa kwa bwana wake, kusudi asikulaani, na kuonekana kwamba uko na kosa. Kuna watu ambao wanalaani baba zao, wala hawana shukrani kwa mama zao. Kuna watu ambao wanajiona kuwa safi, kumbe bado hawajatakaswa uchafu wao. Kuna watu ambao macho yao yanajaa kiburi. Wanazarau kila kitu wanachoona. Kuna watu ambao meno yao ni kama upanga, na mataya yao ni kama visu. Wako tayari kuwatafuna wamasikini wa inchi, na wakosefu wanaokuwa kati ya watu! Muruba ana wabinti wawili wanaosema: “Unipe, Unipe!” Kuna vitu vitatu ambavyo havishibi hata kidogo, hata vitu vine visivyosema: “Inatosha!” Kuzimu, tumbo la mwanamuke tasa, udongo usioshiba maji, na moto usiosema: “Inatosha!” Kama mutu akimuchekelea baba yake na kuzarau utii kwa mama yake, macho yake yataondolewa na kibombobombo wa pori na kuliwa na tai. Kuna mambo matatu yanayokuwa ya ajabu kwangu, hata mambo mane nisiyoyaelewa: njia ya tai katika anga, njia ya nyoka juu ya jiwe, njia ya mashua ndani ya bahari, na njia ya mwanaume kwa mwanamuke. Mwenendo wa mwanamuke mwasherati ni hivi: yeye anakula, anajipanguza mudomo, na kusema: “Sijafanya kosa lolote!” Kuna mambo matatu ambayo yanaitetemesha dunia, hata mambo mane ambayo haiwezi kuyavumilia: mutumwa anayekuwa mufalme; mupumbafu anayeshiba chakula; mwanamuke asiyependwa anayeolewa; na mujakazi anapotwaa nafasi ya bibi yake. Kuna viumbe vine vidogo sana katika dunia, lakini vina akili sana: siafu ni wadudu wasiokuwa na nguvu, lakini wanajiwekea chakula wakati wa kipwa; sungura ni nyama wasiokuwa na uwezo, lakini wanajitengenezea makao chini ya mawe; nzige hawana mufalme, lakini wote wanaenda pamoja kwa vikundi; mujusi, unaweza kumushika katika mukono, lakini anaingia katika nyumba ya kifalme. Kuna viumbe vitatu vyenye mwendo wa kupendeza, hata viumbe vine vyenye mwendo muzuri: simba, ambaye ni nyama mwenye nguvu kuliko wote wala hamwogopi nyama mwingine yeyote, jogoo anayetembea kwa maringo, beberu, na mufalme mbele ya watu wake. Kama umekuwa mupumbafu hata ukajisifu, au kama umekuwa unapanga maovu, chunga mudomo wako. Maana ukigandisha maziwa, utapata siagi; ukimupiga mutu kwenye pua, atatoka damu. Vilevile kuchochea hasira kunaleta ugomvi. Maneno ya mufalme Lemueli. Mashauri aliyopewa na mama yake: Nikuambie nini mwana wangu? Nikuambie nini mwana wangu niliyezaa? Nikuambie nini wewe niliyeomba kwa Mungu? Usimalize nguvu zako kwa wanawake, usiwape mali yako wale wanaoangamiza wafalme. Haifai, ee Lemueli, haifai wafalme kunywa divai, wala wakubwa kutamani vileo. Wakikunywa watasahau maagizo ya sheria, na kuwanyima haki wenye taabu. Umupe mutu anayekaribia kufa kinywaji kikali, uwape divai wale wenye huzuni tele; wakunywe na kusahau umasikini wao, wasikumbuke tena taabu yao. Lakini wewe, useme kwa ajili ya wote wanaokuwa bubu; na kutetea haki za wote wasiojiweza. Sema kwa ajili yao na kuamua kwa haki, linda haki za wamasikini na wakosefu. Muke mwema atapatikana wapi? Bei yake ni kali kuliko ushanga! Mume wake anamwamini kwa moyo na hatakosa faida. Hamutendei mume wake mabaya hata kidogo, lakini anamutendea mazuri maisha yake yote. Anatafuta sufu na kitani, na kufanya kazi kwa mikono yake kwa bidii. Yeye ni kama mashua za biashara: analeta chakula chake kutoka mbali. Anaamuka mbele ya mapambazuko kwa kutayarishia jamaa yake chakula na kuwagawanyia kazi watumishi wake. Anafikiri kununua shamba, kisha analinunua, na kulima zabibu kwa faida ya jasho lake. Yuko tayari kufanya kazi kwa nguvu na kuimarisha mikono yake. Anatambua kwamba shuguli zake zina faida; anafanya kazi hata usiku kwa mwangaza wa taa yake. Anasokota nyuzi kwa mikono yake mwenyewe, kwa vidole vyake mwenyewe anasuka nguo zake. Anafungua mukono wake kwa kuwapa wamasikini, ananyoosha mukono kwa kusaidia wakosefu. Haogopi juu ya jamaa lake wakati wa baridi kali, maana kila mutu yuko na nguo za kutosha. Anajitengenezea matandiko, nguo zake ni za rangi nyeusi-nyekundu za kitani safi. Mume wake ni mutu mwenye kuheshimiwa katika baraza, anapoikaa katikati ya wazee wa inchi. Mwanamuke huyu anatengeneza nguo na kuziuzisha, anawauzishia wachuuzi mikaba. Nguvu na heshima ndizo sifa zake. Anacheka anapofikiri juu ya wakati unaokuja. Anafungua kinywa kwa kusema kwa hekima; anawashauri wengine kwa wema. Anachunguza yote yanayofanyika katika nyumba yake; hakai bure hata kidogo. Watoto wake wanaamuka na kumushukuru, mume wake anaimba sifa zake. Anasema: “Wanawake wengi wametenda mambo ya ajabu, lakini wewe umewashinda wote.” Mapendezi ni udanganyifu na uzuri wa uso haukawii, lakini mwanamuke anayemwogopa Yawe atasifiwa. Jasho lake linastahili kulipwa. Shuguli zake zinapaswa kuheshimiwa popote. Maneno haya ni ya Muhubiri mwana wa Daudi, aliyekuwa mufalme kule Yerusalema. Muhubiri anasema hivi: Bure, bure kabisa. Vyote ni bure! Mwanadamu anafaidia nini kwa jasho lake lote hapa chini ya jua? Kizazi kimoja kinapita na kingine kinakuja, lakini dunia inadumu milele. Jua linachomoza na kutua; linarudi haraka kwa pahali linapotokea. Upepo unavuma tokea kusini, unazunguka mpaka kaskazini. Unazungukazunguka katika mwendo wake, kisha unarudia tena katika muzunguko wake siku zote. Mito yote inatiririkia ndani ya bahari, lakini bahari haijai hata kidogo; kule ambako mito inatiririkia ndiko kule inaendelea kwenda. Mambo yote yanasababisha muchoko, muchoko mukubwa usioelezeka. Jicho halichoki kuona, wala sikio kusikia. Yaliyokuwa ndiyo yatakayokuwa, yaliyotendeka ndiyo yatakayotendeka. Chini ya jua hakuna jambo jipya. Watu wanasema: “Angalia jambo hili ni jipya”, kumbe limekwisha kutendeka zamani za kale. Hakuna mutu anayekumbuka mambo ya zamani, wala atakayekumbuka yatakayotukia kisha. Mimi Muhubiri, nilikuwa mufalme wa Israeli, kule Yerusalema. Nilifanya bidii kuchunguza na kutafuta kwa hekima kila kitu kinachotukia chini ya mbingu. Hiyo ni taabu kubwa ambayo Mungu amewapa wanadamu. Nimeyaona mambo yote yanayofanywa chini ya jua. Yote ni bure sawa na kutaka kukamata upepo! Kitu kilichokunjama hakiwezi kunyooshwa. Kitu kisichokuwa hakiwezi kuhesabiwa. Basi, nikafikiri nikisema: “Nimejipatia hekima nyingi zaidi kupita wote waliopata kutawala Yerusalema mbele yangu. Kweli, ninajua hekima na maarifa ni nini.” Nilifanya bidii kujua umbalimbali kati ya hekima, wazimu na upumbafu. Lakini niligundua kwamba kufanya hivyo ni sawa na kutaka kukamata upepo. Maana katika kuwa na hekima nyingi kuna wasiwasi; na anayeongeza maarifa zaidi anaongeza huzuni zaidi. Basi, nikawaza: “Ngoja nijitumbukize katika raha, nijifurahishe.” Lakini, niligundua kwamba hiyo nayo ni bure. Nikasema juu ya kicheko: “Ni wazimu”, na raha: “Iko na faida gani?” Nilitafuta kwa hekima namna ya kujichangamusha mwili kwa divai na kutenda sawa na wapumbafu. Nilitaka kuona kitu gani ni kizuri kwa wanadamu kufanya wanapoishi maisha yao mafupi hapa chini ya mbingu. Nilifanya mambo makubwa: nilijenga nyumba na kujilimia mashamba ya mizabibu. Nilijifanyia bustani na mashamba ya miti, nikapanda miti ya matunda ya kila aina. Nilijichimbia visima vya maji ya kumwangilia ile miti. Nilinunua watumwa, wajakazi, na wengine wakazaliwa katika nyumba yangu. Nilikuwa na mali mengi, makundi ya ngombe na kondoo wengi kuliko mutu yeyote aliyenitangulia kukaa Yerusalema. Nilijikusanyia feza na zahabu kutoka hazina za wafalme na toka katika majimbo, nami nilipata waimbaji wanaume na wanawake, na wahabara wanaotamaniwa. Nikakuwa mukubwa, mukubwa kuwapita wote waliopata kuwa katika Yerusalema mbele yangu. Na hekima yangu ikakaa ndani yangu. Kila kitu macho yangu yalichokitamani nilikipata. Moyo wangu sikuunyima raha yoyote. Moyo wangu ulifurahia mambo niliyotenda, na hii ilikuwa zawadi ya jasho langu. Kisha nikafikiri juu ya yote niliyokuwa nimefanya kwa mikono yangu, na jinsi nilivyotoa jasho kwa kuyafanya. Nikatambua kwamba yote ni bure sawa na kutaka kukamata upepo. Hakukukuwa faida yoyote chini ya jua. Basi, nikaanza kufikiri maana ya kuwa na hekima, kuwa mwenda-wazimu, na kuwa mupumbafu. Nikajiuliza: “Mufalme mupya anaweza kufanya kitu gani? Atafanya tu kile kilichofanywa mbele yake.” Basi, mimi nikagundua kwamba hekima ni bora kuliko upumbafu, kama vile mwangaza unavyokuwa bora kuliko giza. Mwenye hekima anaona anakokwenda, lakini mupumbafu anatembea katika giza. Hata hivyo, ninajua vilevile kwamba mwisho wao wote wawili ni mumoja. Basi, nikasema ndani ya moyo wangu: “Yatakayomupata mupumbafu yatanipata na mimi vilevile. Kwa nini, basi, nimekuwa na hekima zaidi?” Nikasema ndani ya moyo wangu: “Hayo nayo ni bure.” Maana hakuna anayemukumbuka mwenye hekima, wala anayemukumbuka mupumbafu, maana katika siku zinazokuja wote watasahaulika. Maana mwenye hekima anakufa sawasawa na mupumbafu! Kwa hiyo, nikachukia maisha, maana yote yanayotendeka chini ya jua yalinisikitisha. Yote ni bure sawa na kutaka kukamata upepo. Nikachukia jasho yote niliyotoa hapa chini ya jua, kuona kwamba ilinipasa nimwachie mutu ambaye atatawala nyuma yangu. Tena, ni nani anayejua kwamba atakuwa mwenye hekima au atakuwa mupumbafu? Hata hivyo, yeye atarizi yote niliyofanya kwa kutoa jasho na kutumia hekima yangu hapa chini ya jua. Hayo nayo ni bure. Basi, nilipofikiri tena juu ya jasho yote niliyotoa chini ya jua, nilikata tamaa. Maana, wakati mwingine, mutu ambaye amefanya kazi kwa kutumia hekima, akili na maarifa yake, anamwachia mutu mwingine afurahie matunda ya kazi ambayo hakuitoshea jasho. Hayo nayo ni bure. Ni jambo baya sana. Mutu anafaidia nini kutokana na jasho yake yote, na juhudi anazohangaika nazo chini ya jua? Maisha yake yote yamejaa taabu, na jasho yake ni mahangaiko matupu. Hata usiku akili yake haipumziki! Hayo nayo ni bure. Hakuna kitu kizuri kwa mwanadamu, isipokuwa kula na kunywa na kufurahia matunda ya jasho yake. Hili nalo nimeliona kwamba linatoka kwa Mungu, maana usipojaliwa na Mungu, hauwezi kupata chakula wala kujifurahisha. Mungu anamujalia mutu anayependezwa naye hekima, akili na furaha; lakini anamupa mwenye zambi kazi ya kuvuna na kulundika, kisha Mungu anavipatia yule anayemupendeza. Hayo nayo ni bure sawa na kutaka kukamata upepo. Kuna muda kwa kila kitu, na wakati kwa kila jambo katika dunia: wakati wa kuzaliwa na wakati wa kufa, wakati wa kupanda na wakati wa kuvuna kilichopandwa, wakati wa kuua na wakati wa kuponyesha, wakati wa kubomoa na wakati wa kujenga, wakati wa kulia na wakati wa kucheka, wakati wa kuomboleza na wakati wa kucheza, wakati wa kutupa mawe na wakati wa kukusanya mawe pamoja, wakati wa kukumbatia na wakati wa kutokumbatia, wakati wa kutafuta na wakati wa kupoteza, wakati wa kuchunga na wakati wa kutupa, wakati wa kupasua na wakati wa kushona, wakati wa kukaa kimya na wakati wa kusema, wakati wa kupenda na wakati wa kuchukia, wakati wa vita na wakati wa amani. Mufanya kazi anafaidia nini kutokana na jasho aliyotoa? Mimi nimeiona kazi ambayo mwanadamu amepewa na Mungu. Mungu amefanya kila kitu kikuwe kizuri kwa wakati wake. Ameweka ndani ya moyo wa mwanadamu mawazo juu ya muda usiokuwa na mwisho, lakini mutu hawezi kuelewa mwanzo na mwisho wa matendo ya Mungu. Ninajua kwamba, kwa mwanadamu, kuna jambo moja tu la kumufalia: kufurahi na kujifurahisha kwa muda wote anapoishi. Kama mwanadamu anakula na kunywa na kufurahia matunda ya jasho yake, hayo ni majaliwa ya Mungu. Ninajua kwamba jambo lolote Mungu analotenda linadumu milele. Hakuna kinachoweza kuongezwa wala kupunguzwa. Mungu amefanya mambo yakuwe hivyo kusudi wanadamu wamwogope yeye. Kinachotukia sasa, kilikwisha tukia; kitakachotukia nyuma kilikwisha kutukia. Mungu anafanya kitu kitukie tena na tena. Zaidi ya hayo, nimegundua chini ya jua kwamba uovu unatawala kwa pahali pa haki na sheria. Basi, nikasema ndani ya moyo wangu: “Mungu atawahukumu watu wa haki hata vilevile na waovu, maana amepanga wakati kwa kila jambo na kwa kila kazi.” Nikasema ndani ya moyo wangu: “Mungu anawajaribu wanadamu, kwa kuwaonyesha kwamba wao ni sawa tu na nyama.” Mwisho wa mwanadamu na mwisho wa nyama ni mumoja. Jinsi mwanadamu anavyokufa ndivyo nyama anavyokufa. Wote wanapumua namna ileile; mwanadamu si bora kuliko nyama. Yote ni bure. Wote wanakufa na kwenda kwa nafasi moja. Wote wametoka katika mavumbi na wote watarudi katika mavumbi. Nani anayejua, basi, kama kweli roho ya mutu inapanda juu, na roho ya nyama inashuka chini ndani ya udongo? Basi, nikatambua kwamba hakuna jambo linalokuwa bora zaidi kwa mwanadamu kufanya kuliko kufurahia kazi yake, kwa sababu amepangiwa hivyo. Nani anayeweza kumujulisha mwanadamu yale yatakayokuwa kisha kufa kwake? Kisha nikaona mateso yote yanayofanyika chini ya jua. Watu wanaogandamizwa wanalia machozi, lakini hakuna mutu yeyote anayewafariji. Wagandamizaji wao wana nguvu, ndiyo sababu hakuna wa kuwafariji. Basi, nikafikiri ndani ya moyo kwamba heri wafu waliokwisha kufa kuliko watu wanaokuwa wazima. Lakini heri zaidi kuliko wafu na wanaokuwa wazima, yule ambaye bado hajazaliwa na kuona maovu yote yanayotendeka hapa chini ya jua. Tena nilitambua kwamba mutu anatoa jasho na kutumia ujuzi wake juu ya wivu tu kwa mwenzake. Hayo nayo ni bure sawa na kutaka kukamata upepo. Mupumbafu hafanyi kazi na mwisho anajiua na njaa. Ni afazali kuwa na kidogo tu, pamoja na amani ndani ya moyo, kuliko kutoa jasho kwa ajili ya kukamata upepo. Tena, niliona jambo moja la bure chini ya jua. Nilimwona mutu mumoja anayekuwa peke yake, hana mwana wala ndugu. Hata hivyo, haachi kutoa jasho. Hatosheki hata kidogo na mali yake wala hatulii na kujiuliza: “Ninatoa jasho kwa ajili ya nani na kujizuiza kuwa na raha?” Hayo nayo ni bure. Ni shuguli inayosikitisha. Ni afazali kuwa wawili kuliko mutu kuwa peke yake. Kwa sababu wawili watapata matunda ya jasho yao. Na mumoja akianguka, huyo mwenzake atamusimamisha. Lakini ole wake mutu anayekuwa peke yake akianguka! Huyo hatakuwa na mutu wa kumusimamisha! Vilevile watu wawili wakilala pamoja watapata joto. Lakini mutu akiwa peke yake atajipatia joto namna gani? Mutu akiwa peke yake anaweza kushindwa na adui, lakini wakiwa wawili watashinda adui. Kamba tatu zikisokotwa pamoja hazikatiki upesi. Afazali kijana masikini mwenye hekima kuliko mufalme muzee mupumbafu, ambaye hasikilizi shauri jema, hata ikiwa alikuwa mufungwa na sasa ni mufalme, au alizaliwa masikini na sasa ni mufalme. Niliwaona watu wote wanaoishi chini ya jua wakishikamana na yule kijana ambaye angekamata nafasi ya mufalme. Hesabu ya watu haikukuwa na mwisho, naye aliwatawala wote. Hata hivyo, wale wanaozaliwa nyuma hawatamufurahia. Hakika hayo nayo ni bure sawa na kutaka kukamata upepo. Ukuwe mwangalifu unapokwenda katika nyumba ya Mungu na ukaribie kwa kusikiliza kwa uangalifu, kuliko kutoa sadaka kama vile wapumbafu wanavyofanya, watu wasiojua kwamba wanafanya mabaya. Fikiri mbele ya kusema, wala usikuwe mwepesi kwa kusema neno lolote mbele ya Mungu, kwa maana Mungu yuko mbinguni na wewe uko katika dunia. Kwa hiyo usiseme maneno mengi. Kadiri mutu anavyohangaika zaidi, ndivyo atakavyoota ndoto; sauti ya mupumbafu ni maneno mengi. Ukimutolea Mungu ahadi, usikawie kuitimiza. Mungu hapendezwi na wapumbafu. Timiza kile ulichoahidi. Ni afazali usifanye ahadi kuliko kufanya ahadi kisha usiitimize. Angalia kinywa chako kisikuingize katika zambi, halafu ikupase kumwambia mujumbe wa Mungu kwamba haukukusudia kutenda zambi. Kwa nini kumusukuma Mungu akukasirikie na kuiharibu kazi yako? Ndoto zikizidi, kuna maangamizi na maneno yanakuwa mengi. Jambo la maana ni kumwogopa Mungu. Usishangae ukiona katika inchi wamasikini wanagandamizwa, wananyimwa haki na sheria zao. Kila mwenye cheo anayewatesa wamasikini yupo chini ya mukubwa mwingine, na juu ya hao wote kuna wakubwa zaidi. Faida ya mavuno ya inchi ni kwa watu wote, hata mufalme vilevile anatumainia mavuno yale. Yule anayependa feza hatatosheka na feza, wala anayetamani mali hata akiipata hatatosheka. Hayo nayo ni bure. Mali ikiongezeka, wale watakaoikula wanaongezeka vilevile, naye mwenye mali inamufalia nini isipokuwa kuiangalia tu mali yake? Usingizi wa mutumishi ni mutamu, akuwe ameshiba au amekula kidogo tu. Lakini usingizi wa tajiri ni wa wasiwasi siku zote, maana mali yake inamuzuia kupata usingizi. Tena, nimeona jambo moja ovu sana chini ya jua: mutu alijikusanyia mali, ikakuwa hatari kwake. Kwa bahati mbaya, mali hiyo iliharibiwa katika matumizi mabaya. Kwa mwisho, mutu yule hakukuwa na kitu chochote wakati alipokuwa na mwana. Kama vile mwanadamu alivyokuja katika dunia akiwa uchi toka katika tumbo la mama yake, ndivyo atakavyorudi uchi kule alikotoka. Hataweza kupeleka hata sehemu ndogo ya mapato ya kazi yake. Hili nalo ni jambo baya sana. Atarudi kama vile alivyokuja. Amepata faida gani? Ametoa jasho kwa kukamata upepo. Aliishi maisha yake yote katika giza na huzuni, katika mahangaiko, magonjwa na hasira. Basi, haya ndiyo niliyotambua: jambo zuri na lenye kufaa kwa mwanadamu ni kula, kunywa na kufurahia matunda ya jasho anayotoa hapa chini ya jua, siku zile chache za maisha aliyojaliwa na Mungu, maana hivi ndivyo alivyopangiwa. Kama Mungu anamupa mutu utajiri na mali na kumujalia wakati wa kuyafurahia, basi mwanadamu ashukuru na avifaidie hivyo alivyojipatia kwa jasho lake. Hiyo ni zawadi kutoka kwa Mungu. Na kwa kuwa Mungu amemuruhusu kuwa na furaha, mwanadamu hatakuwa na wasiwasi mwingi juu ya maisha yake mafupi. Nimeona jambo moja ovu hapa chini ya jua, linalowagandamiza watu: Mungu anamujalia mutu utajiri, mali na heshima, hata hakosewi kitu chochote anachotamani, lakini hamupi uwezo wa kuvifurahia vitu hivyo. Pahali pake, mugeni fulani atavifaidia. Hayo nayo ni bure. Ni jambo la mateso mabaya. Mutu akiweza kuzaa watoto mia moja, na akiishi maisha marefu, lakini kama mutu huyo hafurahii maisha yake, wala hafanyiwi mazishi, basi ninasema mutoto aliyezaliwa amekufa ni afazali kuliko mutu yule. Mutoto mufu anakuja kwa bure naye anarudi katika giza, na kusahaulika. Zaidi ya hayo, mutoto wa namna hiyo hakupata kuuona mwangaza wa jua wala kutambua kitu chochote. Hata hivyo, yule mutoto anapumzika kuliko yule mutu. Ingawa mutu huyo ataishi miaka elfu mbili, lakini hafurahii maisha, basi yeye ni kama yule mutoto. Wote wawili wanakwenda fasi moja. Mutu anatoa jasho kwa ajili ya kupata chakula, lakini tamaa yake ya kula haitoshelezwi hata kidogo. Basi mutu mwenye hekima ana faida zaidi kuliko mupumbafu? Na mutu masikini anapata faida gani akijua namna ya kuishi? Hayo nayo ni bure sawa na kutaka kumata upepo. Afazali kufurahia kitu ambacho uko nacho kuliko kuhangaika kwa kutamani kitu kingine. Kila kitu kinachotukia kilikwisha kupangwa tangu zamani. Hali ya mwanadamu inajulikana, na tunajua kwamba muzaifu hawezi kubishana na mutu mwenye nguvu zaidi. Maneno yanapokuwa mengi, ndivyo yanaendelea kuwa bure. Hayana faida. Nani anayejua yanayofaa kwa mutu katika maisha haya mafupi yasiyokuwa na faida, maisha ambayo yanapita kama kivuli? Nani anayejua yale yatakayotukia chini ya jua nyuma ya kufa kwake? Sifa nzuri ni bora kuliko marasi ya bei kali. Siku ya kufa ni bora kuliko siku ya kuzaliwa. Afazali kwenda kwenye kilio, kuliko kwenda kwenye karamu, kwa sababu inawapasa wenye kuwa wazima kukumbuka kwamba kifo kinawangojea sisi wote. Huzuni ni afazali kuliko kicheko, maana, kwa huzuni ya uso moyo unafurahishwa. Moyo wa mwenye hekima uko ndani ya nyumba ya kilio, lakini moyo wa mupumbafu unapenda raha. Afazali kusikia maonyo ya wenye hekima kuliko kusikiliza nyimbo za wapumbafu. Maana, kicheko cha mupumbafu ni kama mulio wa miiba katika moto. Hayo nayo ni bure. Mwenye hekima akimutesa mutu, yeye anafanya kama mupumbafu. Kupokea kituliro kunapotosha akili. Mwisho wa jambo ni afazali kuliko mwanzo wake. Moyo muvumilivu ni bora kuliko moyo wa majivuno. Usikuwe mwepesi wa hasira, maana, hasira inakaa ndani ya wapumbafu. Usiulize: “Kwa nini nyakati za zamani zilikuwa bora kuliko za sasa?” Hauulizi hivyo kwa kutumia hekima. Hekima ni ya bei kubwa kama urizi; ni ya mafaa kwa wale wote wanaokuwa wazima. Kulindwa na hekima ni kama kulindwa na feza. Faida ya maarifa ni kwamba hekima inalinda maisha ya mutu anayekuwa nayo. Mufikiri vema juu ya kazi ya Mungu. Ni nani anayeweza kunyoosha kitu Mungu alichokunja? Katika siku za kufanikiwa ukuwe na furaha. Katika siku za hasara ufikiri juu ya jambo hili: Mungu amefanya hiyo ya kwanza iambatane na ya pili kusudi mwanadamu asipate kujua mambo yatakayotukia nyuma yake. Katika maisha yangu ya bure, niliona kila kitu. Mutu wa haki anakufa ingawa ni wa haki, ambapo mutu mwovu anaendelea kuishi maisha marefu ingawa ni mwovu. Basi, usikuwe wa haki kupita kipimo, wala usikuwe mwenye hekima zaidi! Kwa nini kujiangamiza wewe mwenyewe? Lakini vilevile, usikuwe mwovu sana wala usikuwe mupumbafu! Kwa nini kufa mbele ya wakati wako? Inakupasa ushike neno la kwanza na la pili vilevile; maana anayemutii Mungu atayaepuka yote. Hekima inamufanya mwenye hekima kuwa na nguvu zaidi kuliko watawala kumi katika muji. Hakika, hakuna mutu wa haki katika dunia anayetenda vizuri siku zote bila kutenda zambi. Usifuate maneno yote wanadamu wanayosema, kusudi usisikie mutumishi wako akikutukana. Wewe mwenyewe unajua ndani ya moyo kwamba umetukana wengine mara nyingi. Nimeyapima yale yote kwa hekima; nikajisemesha: “Ninataka kuwa mwenye hekima!” Lakini hekima iko mbali sana nami. Jinsi gani mwanadamu ataweza kutambua maana ya maisha? Jambo hilo ni zito na gumu sana kwetu. Hata hivyo, nilikusudia kujua na kuchunguza na kutafuta hekima na maana ya mambo yanayokuwa, na vilevile kujua kwamba uovu ni upumbafu na kwamba upumbafu ni wazimu. Jambo moja nililotambua linalokuwa baya zaidi kuliko kifo, ni mwanamuke ambaye moyo wake ni mutego na wavu, na mikono yake ni kama minyororo. Lakini anayemupendeza Mungu anamwepuka mwanamuke yule, lakini mwenye zambi ananaswa naye. Ninakuambia mimi Muhubiri, haya ndiyo niliyotambua nilipofanya uchunguzi wangu kidogokidogo. Niliendelea kutafuta mambo hayo, lakini sikupata. Kati ya wanaume elfu moja, nilipata kuona mwanaume mumoja anayestahili heshima, lakini kati ya wanawake wote, sikuona hata mumoja anayestahili heshima. Nimetambua jambo hili moja: kwamba Mungu aliwaumba wanadamu wenye usawa, lakini wao wenyewe wamejitafutia matatizo. Nani anayekuwa kama mwenye hekima? Nani anayejua maana ya kila kitu? Hekima inaangarisha uso wa mutu, inaondoa alama za upumbafu. Mimi ninasema hivi: tii amri ya mufalme. Kwa sababu ya kiapo chako kitakatifu, usikate tamaa. Usifanye haraka kukataa mamlaka yake, wala usiendelee kutenda lisilomupendeza, maana mufalme anafanya jinsi anavyopenda. Amri ya mufalme ni shauri la mwisho. Nani anayesubutu kumwuliza: “Unafanya nini?” Anayetii amri hatapata hasara, na mwenye hekima atajua kwamba kuna wakati wa hukumu. Kweli, kila kitu kina wakati wake na njia yake, ingawa mwanadamu anapatwa na tatizo kubwa. Hajui ni kitu gani kitakachotukia nyuma, maana ni nani anayeweza kumujulisha yatakayotukia nyuma? Hakuna mutu anayekuwa na uwezo wa kushikilia roho yake kusudi asikufe; hakuna mutu anayekuwa na uwezo juu ya siku ya kufa. Wakati wa vita hakuna kuponyoka, na uovu hauwezi kumwokoa mwovu. Haya yote nimeyaona katika uchunguzi wangu juu ya yote yanayotendeka hapa chini ya jua, ambako mwanadamu anatawala mwenzake na kumutesa. Tena, nimeona waovu wakizikwa, watu ambao walizoea kuingia na kutoka pahali patakatifu, na kusifiwa katika muji uleule walimotenda maovu yao. Hayo nayo ni bure. Kwa vile uovu hauazibiwi haraka, mioyo ya wanadamu inakusudia kutenda mabaya. Wenye zambi wanatenda maovu mara mia. Hata hivyo, wanaendelea kuishi. Lakini, mimi ninajua kwamba itakuwa heri kwa wanaomwogopa Mungu, kwa sababu ya woga wao. Lakini hakuna furaha kwa waovu. Wao watapita kama kivuli, maisha yao hayatakuwa marefu kwa sababu hawamwogopi Mungu. Kuna jambo moja la bure nililotambua hapa katika dunia: mara kwa mara watu wema wanatendewa jinsi waovu wanavyostahili kutendewa, nao waovu wanatendewa jinsi watu wema wanavyostahili kutendewa. Ninasema kwamba hayo nayo ni bure. Basi, mimi ninasifu furaha, kwa maana hapa chini ya jua hakuna kitu kinachokuwa kizuri zaidi kuliko kula na kunywa na kujifurahisha. Haya ndiyo mutu anayoweza kufanya anapotoa jasho katika muda wa maisha yake aliyojaliwa na Mungu chini ya jua. Kila mara nilipojitoa kwa kujua hekima na kuona yanayotendeka hapa katika dunia, nilitambua kwamba mutu anaweza kukaa macho muchana na usiku, lakini hataelewa kazi ya Mungu inayofanyika chini ya jua. Mutu anaweza kutoa jasho sana lakini hataelewa. Wenye hekima wanaweza kujidai kwamba wanajua, lakini, kwa kweli, hawajui. Nilifikiri sana juu ya hayo yote, nikaona kwamba Mungu anaongoza matendo ya watu wenye hekima na wenye haki; ikiwa ni upendo au chuki, mwanadamu hajui. Kila kitu kwao ni bure, maana mwisho uleule unawapata wenye haki na waovu, wazuri na wabaya, wanaohesabiwa kuwa safi na wachafu, wenye kutoa sadaka na wasiotoa sadaka. Mutu muzuri ni sawa tu na mwenye zambi, na mwenye kuapa si tofauti na asiyeapa. Hili ni jambo baya zaidi kati ya yote yanayotukia hapa chini ya jua, kwamba mwisho uleule unawapata wote. Tena, wakati wote wa maisha yao, wanadamu wanajaa uovu na wazimu, na kisha wanakufa. Lakini anayeambatana na wanaoishi angali bado na tumaini. Afazali imbwa mwenye kuishi kuliko simba mwenye kufa. Maana, wanaoishi wanajua kwamba watakufa, lakini wafu hawajui kitu chochote. Hawana malipo tena. Hakuna ukumbusho juu yao, wamesahauliwa kabisa. Upendo wao, chuki zao na tamaa zao, vyote vimetoweka pamoja nao, wala hawatashiriki tena katika kitu chochote hapa chini ya jua. Kwenda ukule chakula chako kwa furaha, na ukunywe divai yako kwa moyo wenye kuchangamuka, maana Mungu amekwisha kukubali kazi yako. Vaa vizuri, ujipakae mafuta kwenye kichwa. Furahia maisha pamoja na muke wako unayemupenda muda wote wa maisha yako ya bure ambayo Mungu amekujalia hapa chini ya jua, maana hilo ndilo ulilopangiwa katika maisha, katika kutoa jasho yako hapa chini ya jua. Kila kitu unachotaka kufanya ukifanye kwa nguvu zako zote, maana, hakuna kazi, wala wazo, wala maarifa, wala hekima kule katika kuzimu unakokwenda. Tena, nimeona kitu kimoja hapa chini ya jua, kwamba wenye kukimbia mbio hawashindi katika mashindano ya kukimbia, wala wenye nguvu hawashindi vita, wenye hekima hawapati chakula, wenye akili hawatajiriki, wala wenye ujuzi hawapandi vyeo. Lakini wakati wa bahati unawapata wote pamoja. Mutu hajui saa yake itafika wakati gani. Kama vile samaki wanavyonaswa katika wavu kwa bahati mbaya, na kama vile ndege wanavyonaswa katika mutego kwa rafla, ndivyo wanadamu wanavyonaswa na hasara inapowaangukia bila kutazamia. Vilevile hapa chini ya jua nimeona mufano wa hekima, na ulionekana kwangu kuwa wenye maana sana. Kulikuwa muji mumoja mudogo wenye wakaaji wachache. Mufalme mumoja mwenye nguvu akafika, akauzunguka na kujitayarisha kuushambulia. Katika muji ule, kulikuwa masikini mumoja mwenye hekima ambaye, kwa hekima yake, aliokoa muji ule. Lakini hakuna mutu aliyemukumbuka yule masikini kisha. Basi, mimi ninasema, hekima ni bora kuliko nguvu, ingawa hekima ya masikini inazarauliwa, na maneno yake hayasikilizwi. Afazali kusikiliza maneno matulivu ya mwenye hekima, kuliko kusikiliza kelele za mufalme katika kikao cha wapumbafu. Kuwa na hekima ni bora kuliko kutegemea silaha, lakini mwenye zambi mumoja anaharibu mazuri mengi. Mainzi waliokufa wanaharibu na kunukisha marasi; upumbafu kidogo unapoteza hekima na heshima. Moyo wa mwenye hekima unamwongoza kutenda mambo yanayokuwa sawa; lakini mutu mupumbafu anapotoshwa na moyo wake. Hata anapopita katika njia, anakosa akili, anamwambia kila mutu kwamba yeye ni mupumbafu. Mutawala akikukasirikia, usiache kazi; makosa makubwa yanaweza kufutwa ukiwa munyenyekevu. Kuna uovu niliotambua hapa chini ya jua, uovu unaosababishwa na watawala: wapumbafu wanapewa kazi za madaraka ya juu, na watajiri wanakamata nafasi za mwisho. Nimeona watumwa wanapanda juu ya farasi, na wakubwa wanatembea kwa miguu kama watumwa. Yeye anayechimba shimo anatumbukia ndani yake mwenyewe, anayebomoa ukuta anaumwa na nyoka. Muchonga mawe anaumizwa nayo, mukata kuni anapatwa na hatari. Nguvu nyingi zaidi zinahitajika kwa mutumiaji wa shoka lisilonolewa, lakini kutumia hekima kunamufanya mutu afanikiwe. Nyoka ya muchawi ikiuma mbele haijachochewa, hakuna faida tena kwa muchawi. Maneno ya mwenye hekima yanamupa upendeleo; lakini maneno ya mupumbafu yanamwangamiza. Mupumbafu anaanza kusema kwa maneno ya kijinga, na kumaliza masemi yake kwa wazimu wa hatari. Mupumbafu anasema maneno mengi. Mwanadamu hajui yatakayokuwa, wala yale yatakayotukia nyuma yake. Mupumbafu anachokeshwa kwa kutoa jasho, hata hajui njia ya kwenda katika muji. Ole wako, ewe inchi, mutawala wako akiwa kijana, na viongozi wako wakifanya karamu asubui. Heri yako, ewe inchi, mutawala wako akiwa mutu wa heshima, na viongozi wako wakifanya karamu wakati unaofaa, kwa kujipatia nguvu na si kujilewesha. Kutokana na uvivu wa mutu, paa ya nyumba inaanguka; kwa sababu ya uregevu, nyumba inavuja. Chakula ni kwa ajili ya kujifurahisha, divai inachangamusha maisha, na feza inasababisha hayo yote. Usimutukane mutawala hata ndani ya moyo wako, wala usimutukane tajiri hata ndani ya chumba chako cha kulala, maana ndege atapeleka sauti yako, kiumbe kinachoruka kitatangaza maneno yako. Tupa chakula chako juu ya maji. Nyuma ya siku nyingi utakipata tena! Gawa sehemu moja kwa watu saba hata wanane, maana, haujui hasara itakayofika katika dunia. Mawingu yakijaa maji, mvua inanyesha. Muti ukiangukia upande wa kusini au wa kaskazini, pale unapoangukia ndipo unapolala. Anayechunguza upepo hatapanda mbegu, anayeangalia mawingu yatoweke, hatavuna kitu. Kama vile hauwezi kujua jinsi uzima unavyoingia katika mifupa ya mutoto katika tumbo la mama yake, vilevile hauwezi kuelewa matendo ya Mungu, aliyefanya kila kitu. Panda mbegu asubui na usiache kupanda mpaka magaribi, maana, haujui mbegu gani zitaota; za asubui, za magaribi, au zote zitakuwa nzuri. Mwangaza ni muzuri, na kuona jua kunapendeza macho. Mutu akiishi miaka mingi, afurahie miaka hiyo yote; lakini akumbuke kwamba siku mbaya zitakuwa nyingi, na kwamba yote yatakayofuata ni bure. Ewe kijana, furahia ujana wako, moyo wako ukuwe na raha wakati ungali kijana. Fuata mapenzi ya moyo wako na tamaa ya macho yako. Lakini kumbuka kwamba Mungu atakuhukumu kadiri ya hayo yote. Ondoa mahangaiko ndani ya moyo wako, ujikinge usipate maumivu katika mwili kwa sababu ujana na nguvu vinapita mbio. Ukumbuke Muumba wako siku za ujana wako wakati hazijafika siku mbaya wala haijakaribia miaka utakaposema: “Sina furaha katika vitu hivyo.” Kwa wakati huu wa nyuma, jua, mwangaza, mwezi na nyota hazionekani tena, mawingu yanarudia nyuma ya mvua, walinzi wa nyumba wanatetemeka, wenye nguvu wanakunjama, wasagaji wanaacha kazi kwa sababu ni wachache, wanaochungulia kwenye dirisha wanakuwa zaifu, milango imefungwa, sauti za visagio zimekuwa ndogo, watu wanashituliwa na sauti ya ndege, sauti za muziki zimekuwa ndogo, watu wanaogopa mupando na kutishwa katika njia, muti wa lozi unachanua maua yake meupe, mapanzi hayawezi kuruka, hakuna hamu tena, mwanadamu anaelekea kwenye makao yake ya milele, waombolezaji wanasambaa katika njia, uzi wa feza unakatika kikombe cha zahabu kinapondekana, mutungi wa maji unavunjikia kwenye chemichemi, gurudumu la kukokota maji linavunjika kwenye kisima, mavumbi yanarudilia inchi tena, na roho inamurudilia Mungu aliyeipana. Muhubiri anasema hivi: Bure, bure kabisa. Vyote ni bure. Basi, zaidi ya kuwa na hekima yake, Muhubiri aliendelea kuwafundisha watu ujuzi. Alipima, akachunguza na kutia kwa usawa mezali kwa ufundi mwingi. Muhubiri alijikaza kupata maneno ya kupendeza, akaandika kwa usawa maneno ya kweli. Misemo ya wenye hekima ni kama fimbo ya kuongoza ngombe. Mezali zilizokusanywa pamoja na muchungaji mumoja ni kama misumari iliyopigiliwa kwa nguvu. Zaidi ya hayo, mwana wangu, ujilinde! Kuandika vitabu hakuna mwisho na kusoma kwingi kunachokesha mwili. Nyuma ya hayo yote yaliyokwisha kusemwa, kungali hili linalotakiwa: Umwogope Mungu, na ushike amri zake, kwa sababu hayo ndiyo mapaswa ya mwanadamu. Maana, Mungu atahukumu matendo yote, hata yale yanayotendwa kwa siri, yakuwe mazuri au mabaya. Wimbo wa Solomono unaokuwa bora kuliko nyimbo zote. Heri midomo yako ingalinibusu, maana mapendo yako ni bora kuliko divai. Manukato yako yananuka vizuri, na jina lako ni kama marasi yenye harufu nzuri. Kwa hiyo wabinti wote wanakupenda! Unipeleke, tuende haraka, mufalme amenileta katika chumba chake. Tutafurahi na kukushangilia pamoja, tutasifu mapenzi yako kuliko divai. Wabinti wana haki ya kukupenda! Enyi wabinti wa Yerusalema, mimi ni mweusi. Ninapendeza kama mahema ya Kedari, kama mapazia ya nyumba ya Solomono. Musinishangae kwa sababu mimi ni mweusi. Ni kwa sababu jua limenichoma. Wandugu zangu walinikasirikia, wakanifanya kuwa mutumishi katika mashamba ya mizabibu. Lakini sikuchunga shamba langu la mizabibu. Basi uniambie ee wangu wa moyo, utawakulishia kondoo wako wapi? Ni wapi watakapopumzikia pa saa sita? Kwa nini mimi nikutafute kati ya makundi ya wenzako? Ewe unayependeza kuliko wanawake wote; kama haujui, fanya hivi: ufuate nafasi kondoo walipopita; basi, uwakulishie mbuzi wako karibu na hema za wachungaji. Wewe ee mupenzi wangu, ninakulinganisha na farasi dume wa magari ya Mufalme wa Misri. Pete za masikio zinapendeza mashavu yako. Mikufu ya mawe ya bei kali inapendeza shingo yako. Tutakufanyizia mikufu ya zahabu, iliyopambwa vizuri kwa feza. Mufalme alipokuwa akiikaa kwenye meza yake, marasi yangu ya nardo yalisambaa kila pahali. Mupenzi wangu ni kama mufuko wa ubani kwangu, kati ya maziba yangu. Mupenzi wangu ni kama maua ya hina yanayochanua kwenye mashamba ya mizabibu kule Engedi. Hakika sura yako ni nzuri, ee mupenzi wangu, hakika sura yako ni nzuri! Macho yako ni kama ya njiwa! Hakika sura yako ni nzuri, ewe ninayekupenda, sura yako ni nzuri kweli! Majani mabichi yatakuwa kitanda chetu; miti ya mierezi itakuwa nguzo za nyumba yetu, na miti ya miberoshi itakuwa dari yake. Mimi ni kama ua la Saroni, ni yungiyungi ya mabonde. Kama yungiyungi kati ya michongoma, ndivyo mupenzi wangu anavyokuwa kati ya wabinti. Kama muti wa matunda kati ya miti ya pori, ndivyo mupenzi wangu anavyokuwa kati ya vijana. Ninafurahia kuikaa chini ya kivuli chake, na tunda lake tamu sana kwangu. Alinipeleka mpaka katika chumba cha karamu, akapandisha bendera ya mapenzi juu yangu. Munishibishe na zabibu kavu, munifurahishe kwa matunda, maana ninaugua kwa mapenzi! Mukono wake wa kushoto uko chini ya kichwa changu, mukono wake wa kuume unanikumbatia. Ninawasihi, enyi wabinti wa Yerusalema, kama vile paa au swala wanavyokuwa katika pori, musichochee wala kuamusha mapenzi, mpaka pale wakati wake utakapofika. Hiyo ni sauti ya mupenzi wangu, yeye anakuja mbio, anaruka milima, vilima anavipita haraka! Mupenzi wangu ni kama paa, ni kama swala muchanga. Anasimama karibu na ukuta wetu, anachungulia kwenye dirisha, anaangalia kwenye wavu. Mupenzi wangu ananiambia, akisema: Simama basi, ewe mupenzi wangu, unayependeza, kuja tuende zetu. Wakati wa baridi umepita, nazo mvua zimekwisha kukoma; maua yamechanua kila pahali. Wakati wa kuimba umefika; sauti za njiwa zinasikilika katika mashamba yetu. Miti ya tini imeanza kuzaa na mizabibu imechanua. Inatoa harufu nzuri. Kuja, basi, ewe mupenzi wangu unayenipendeza, kuja tuende. Ee njiwa yangu, uliyejificha katika matundu kwenye mulima, uniache kuona uso wako na kusikia sauti yako, maana sauti yako ni nzuri na uso wako unapendeza. Mutukamatie mbweha, wale mbweha wadogowadogo, wanaoharibu mizabibu yetu inayochanua. Mupenzi wangu ni wangu, nami ni wake. Yeye anakulisha kondoo wake penye yungiyungi. Mpaka pale jua linapochomoza na vivuli kutoweka, rudi kama paa, mupenzi wangu, kama swala mudogo juu ya milima ya Beteri. Usiku nikiwa kwenye kitanda changu, nilimutafuta yule ninayemupenda. Nilimutafuta, lakini sikumupata. Nikaamuka, nikazunguka katika muji, katika barabara na nafasi za makutano, nikimutafuta yule wangu wa moyo. Nilimutafuta, lakini sikumupata. Walinzi wa muji waliniona walipokuwa wanazunguka katika muji. Basi nikawauliza: Mumemwona mupenzi wangu wa moyo? Mara tu nilipoachana nao, nikamwona mupenzi wangu wa moyo. Nikamushika wala sikumwacha aondoke, mpaka nilipomupeleka katika nyumba kwa mama yangu, mpaka ndani ya chumba cha yule aliyenizaa. Ninawasihi, enyi wabinti wa Yerusalema, kama vile paa au swala wanavyokuwa katika pori, musichochee wala kuamusha mapenzi, mpaka pale wakati wake utakapofika. Ni kitu gani kile kinachotoka katika jangwa kama munara wa moshi, kinachotoa harufu ya manemane na ubani, manukato yanayouzishwa na wachuuzi? Angalia! Ni kipoyi cha Solomono, akibebwa juu ya kiti chake cha kifalme, akizungukwa na walinzi makumi sita, mashujaa bora wa Israeli. Kila mumoja wao ameshika upanga, kila mumoja wao ni hodari wa vita. Kila mumoja ana upanga wake kwenye kiuno, tayari kupambana na adui usiku. Mufalme Solomono alijitengenezea kipoyi, kwa mbao nzuri kutoka Lebanoni. Nguzo zake zilitengenezwa kwa feza, nafasi ya kuegemea imefunikwa kwa zahabu, nafasi ya kuikalia imefunikwa na vitambaa vya nyekundu-nyeusi. Katikati yake kilipambwa na wabinti wa Yerusalema waliokishonea vitambulisho vya upendo. Mukuje basi enyi wabinti wa Sayuni, mumwone mufalme Solomono. Amevaa taji aliyovalishwa na mama yake, siku alipofanya ndoa yake, siku ambayo moyo wake ulijaa furaha. Hakika sura yako ni nzuri, ewe mupenzi wangu, hakika sura yako ni nzuri! Macho yako ni mazuri kama ya njiwa ndani ya ushungi wako. Nywele zako ni kama kundi la mbuzi wanaoshuka kwenye milima ya Gileadi. Meno yako ni kama kundi la kondoo dike waliokatwa manyoya, wanaotoka kwenye maji kisha kuogeshwa; kila mumoja akiwa na pacha lake, na hakuna yeyote aliyekufiwa. Midomo yako ni kama utepe mwekundu, kinywa chako kinapendeza kweli. Mashavu yako ni kama nusu mbili za makomamanga ndani ya ushungi wako. Shingo yako ni kama munara wa Daudi, uliojengwa kwa kulinda silaha, ambako ngao elfu moja zimetundikwa, zote zikiwa za mashujaa. Maziba yako ni kama paa mapacha, ambao wanachungwa penye yungiyungi. Nitakaa kwenye mulima wa marasi, na kwenye kilima cha ubani, mpaka pale kutakapopambazuka, na giza kutoweka. Wewe ni nzuri kabisa, ee mupenzi wangu, wewe hauna kilema chochote. Kuja, muchumba wangu, tuondoke Lebanoni, na tuiache mbali milima ya Lebanoni. Shuka toka kilele cha mulima Amana, toka kilele cha Seniri na Hermoni, toka mashimo ya simba, toka kwenye milima ya chui. Umeua moyo yangu, dada yangu, muchumba wangu, umeua moyo yangu, kwa kunitupia jicho mara moja tu, na kwa ule mukufu wako katika shingo. Dada yangu, muchumba wangu; mapendo yako yananivuta ajabu. Ni bora kuliko divai, marasi yako yananuka vizuri kuliko viungo vyote. Midomo yako inadondosha asali, ee muchumba wangu, ulimi wako una asali na maziwa. Harufu nzuri ya nguo zako ni kama miti ya Lebanoni. Dada yangu, muchumba wangu, ni bustani yangu ya pekee, chemichemi inayochungwa. Machipukizi yako ni bustani ya mikomamanga pamoja na matunda bora kuliko yote, hina na nardo, nardo na zafarani, muchai na mudalasini, ubani na udi, na mimea mingine yenye harufu nzuri. Wewe ni chemichemi ya bustani, kisima cha maji yasiyokauka, vijito vinavyotiririka kutoka milima ya Lebanoni. Vuma, ewe upepo wa kaskazini, kuja, ewe upepo wa kusini, muvume juu ya bustani yangu, mujaze anga kwa marasi, mupenzi wangu akuje katika bustani yake akule matunda yake bora kuliko yote. Ninaingia katika bustani yangu, dada yangu, muchumba wangu. Ninakusanya manemane na majani yenye harufu, ninakula sega langu la asali, ninakunywa divai yangu na maziwa yangu. Mukule, enyi warafiki, mukunywe; mukunywe sana, wapendwa wangu. Nililala usingizi, lakini moyo wangu ulikesha. Nikasikia mupenzi wangu akipiga hodi. Unifungulie dada, ee mupenzi wangu, muchumba wangu, njiwa yangu, usiyekuwa na kilema chochote. Kichwa changu kimelowana na umande na nywele zangu na manyunyu ya usiku. Nimekwisha kuvua nguo zangu, nitazivaa namna gani tena? Nimekwisha kunawa miguu yangu, niichafue namna gani tena? Halafu mupenzi wangu akaugusa mulango, moyo wangu ukajaa furaha. Nikasimama kwa kumufungulia mupenzi wangu. Mikono yangu ikajaa manemane, na vidole vyangu vikadondosha manemane, nikashika kifungio kwa kufungua mulango. Nikamufungulia mupenzi wangu mulango, lakini kumbe, alikuwa amekwisha kutoweka. Moyo wangu ulifurahi alipokuwa akizungumuza! Nikamutafuta, lakini sikumupata; nikamwita, lakini hakuniitikia. Walinzi wa muji walinikuta, walipokuwa wakizunguka katika muji. Wakanipiga na kuniumiza; nao walinzi wa mulango wakaninyanganya ushungi wangu. Ninawasihi, enyi wabinti wa Yerusalema, mukimwona mupenzi wangu, mumwelezee kwamba ninaugua kwa ajili ya mapenzi! Ewe unayependeza kuliko wabinti wote, huyo mupenzi wako ana nini cha zaidi ya mupenzi mwingine, hata utusihi kwa moyo mpaka pale? Mupenzi wangu ni muzuri na ni mwekundu, anatambulikana kati ya wanaume elfu kumi. Kichwa chake ni kizuri kama zahabu safi, nywele zake ni zenye kulembelea, nyeusi sana kama kibombobombo. Macho yake ni kama ya njiwa kandokando ya kijito, ni kama njiwa waliooga maziwa pembeni ya kijito. Mashavu yake ni kama bustani inayojaa marasi, yenye harufu nzuri. Midomo yake ni kama yungiyungi, inatonatona manemane kwa wingi. Mikono yake ni kama pete za zahabu, amevaa mawe ya bei kali. Kiwiliwili chake ni kama pembe za tembo zilizopambwa kwa mawe ya yakuti ya rangi ya samawi. Miguu yake ni kama nguzo za mawe meusi, zilizosimikwa katika misingi ya zahabu. Umbo lake ni kama mulima Lebanoni, ni bora kama miti ya mierezi. Kinywa chake kinajaa maneno matamu. Yeye wote anapendeza. Basi, hivi ndivyo mupenzi wangu anavyokuwa, ndivyo rafiki yangu anavyokuwa, enyi wabinti wa Yerusalema. Ewe mwanamuke unayekuwa muzuri sana, amekwenda wapi yule mupenzi wako? Ameelekea wapi mupenzi wako, kusudi tupate kushirikiana nawe kwa kumutafuta? Mupenzi wangu amekwenda katika bustani yake, pahali ambapo miti ya marasi inastawi. Yeye anakulisha kondoo wake na kukusanya mayungiyungi. Mimi ni wa mupenzi wangu, naye ni wangu; yeye anawakulisha kondoo wake kwenye mayungiyungi. Mupenzi wangu, sura yako ni nzuri kama muji wa Tirza, unapendeza kama Yerusalema, unatisha kama jeshi lenye bendera. Usiniangalie, tafazali; maana macho yako yananitisha. Nywele zako ni kama kundi la mbuzi wanaoshuka kwenye milima ya Gileadi. Meno yako ni kama kundi la kondoo dike wanaotoka kwenye maji kisha kuogeshwa, kila mumoja akiwa na pacha lake, na hakuna yeyote aliyekufiwa. Mashavu yako ni kama nusu mbili za makomamanga ndani ya ushungi wako. Kuna malkia makumi sita, wahabara makumi nane, na wabinti wasiohesabika! Hakuna anayekuwa sawa njiwa yangu. Anaenea kabisa. Ni kipenzi cha mama yake, ni binti wake pekee. Wabinti wanamwangalia na kumwita mwenye heri, nao malkia na wahabara wanaimba sifa zake. Ni nani huyu anayeonekana kama mapambazuko, muzuri kama mwezi, mwenye kungaa kama jua, na anatisha kama jeshi lenye bendera? Nimeingia katika bustani ya miti ya lozi, kuangalia vichipukizi katika bonde, kuona kama mizabibu imechanua, na mikomamanga imechanua maua. Bila kutazamia, mupenzi wangu akanitia katika gari la mukubwa. Rudia, rudia ewe binti Musulami. Rudia, rudia tupate kukuangalia. Kwa nini munataka kumwangalia Musulami sawa vile munaangalia muchezo wa ngoma kati ya makundi mawili? Miguu yako inapendeza sana katika viatu, ewe binti wa kifalme. Mizunguko ya kiuno chako ni kama ushanga, kazi ya fundi hodari. Kitofu chako ni kama bakuli lisilokosa divai iliyokolezwa. Tumbo lako ni kama lundo la ngano lililozungushiwa mayungiyungi pembeni. Maziba yako ni kama paa mapacha, ni kama swala wawili. Shingo yako ni kama munara wa pembe za tembo. Macho yako ni kama visima vya muji wa Hesiboni, karibu na mulango wa Beti-Rabi. Pua yako ni kama munara wa Lebanoni, ambao unauelekea muji wa Damasiki. Kichwa chako ni kama mulima Karmeli. Misuko ya nywele zako ni nyekundu-nyeusi. Uzuri wako unaweza kumuvuta hata mufalme. Angalia jinsi sura yako ni nzuri na ya kuvutia, ewe mupenzi, binti unayependeza! Umbo lako linapendeza kama muti wa ngazi, maziba yako ni kama shada za ngazi. Nilisema nitapanda muti wa ngazi na kuchuma shada za ngazi. Kwangu maziba yako ni kama shada za zabibu, harufu nzuri ya pumzi yako ni kama matunda ya mutofaa; na kinywa chako ni kama divai tamu. Basi, divai itiririke mpaka kwa mupenzi wangu, ipite juu ya midomo yake na meno yake! Mimi ni wa mupenzi wangu, naye ananisikilia hamu sana. Kuja, ewe mupenzi wangu, tuende katika mashamba, tuende tulale kule katika vijiji. Tutaamuka mapema, tuende kwenye mashamba ya mizabibu, tuone kama imeanza kuchipuka, na kama maua ya zabibu yamekwisha kuchanua, vilevile kama mikomamanga imeanza kutoa maua. Kule ndiko nitakapokupatia pendo langu. Harufu nzuri ya dudai imejaa katika hewa. Karibu na milango yetu kuna kila aina ya matunda bora, yote mapya na ya siku za nyuma, ambayo nimekuwekea wewe mupenzi wangu. Heri ungekuwa kaka yangu, ambaye amenyonyeshwa na mama yangu! Hivyo, hata kama ningekutana nawe inje, ningekubusu na hakuna ambaye angenizarau. Ningekuongoza na kukufikisha ndani ya nyumba ya mama muzazi, pahali ambapo ungenifundisha upendo. Ningekupa divai nzuri iliyokolezwa, ningekupa divai yangu ya makomamanga yangu. Mukono wake wa kushoto uko chini ya kichwa changu, mukono wake wa kuume unanikumbatia. Ninawasihi, enyi wabinti wa Yerusalema, musichochee wala kuamusha mapenzi, mpaka wakati wake utakapofika. Ni nani huyu anayekuja kutoka katika jangwa, akimwegemea mupenzi wake? Mimi nilikuamusha chini ya muti wa mutofaa, pale ambapo mama yako aliona uchungu, pale ambapo mama yako alikuzaa. Unipige kama muhuri ndani ya moyo wako, kama muhuri katika mikono yako. Maana mapendo yana nguvu kama kifo, nao wivu ni mukali kama kaburi. Kuwaka kwake ni kama kuwaka kwa moto, unawaka kama ulimi wa moto. Maji mengi hayawezi kuyazimisha hata kidogo, mafuriko hayawezi kuyazimisha. Mutu akijaribu kununua mapenzi, na kutoa mali yake yote, atakachopata ni mazarau mutupu. Tuna dada mudogo, ambaye bado hajaota maziba. Basi, tutamufanyia dada yetu nini siku atakapochumbiwa? Kama angalikuwa ukuta, tungalimujengea munara wa feza; na kama angalikuwa mulango, tungaliupigilia kwa mbao za mierezi. Mimi nilikuwa ukuta, na maziba yangu kama minara yake. Mbele yake nilikuwa kama mwenye kupata amani. Solomono alikuwa na shamba la mizabibu, pahali panapoitwa Bali-Hamoni. Alilipangisha kwa walinzi; kila mumoja wao alilipa vikoroti elfu moja vya feza. Shamba langu la mizabibu ni shamba langu mwenyewe. Basi, Solomono, wewe ukae na elfu zako za feza, na kila mulinzi wa matunda akae na mia mbili zake. Ewe unayekuwa katika shamba, warafiki zangu wanasikiliza sauti yako; basi nami niisikilize tafazali! Kuja mbio, ewe mupenzi wangu, kama paa au kitoto cha pongo juu ya milima ya marasi. Haya ni maono Isaya mwana wa Amozi, aliyoyaona juu ya inchi ya Yuda na Yerusalema, katika nyakati za utawala wa wafalme hawa wa Yuda: Ahazi na Hezekia. Yawe anasema hivi: Sikiliza enyi mbingu, tega sikio ee dunia. Mimi nimewalea watoto wangu na kuwakomalisha, lakini sasa wameniasi! Ngombe anamufahamu mwenye naye, punda anajua kibanda cha bwana wake; lakini Waisraeli hawajui, watu wangu, hawaelewi! Ole kwako wewe taifa lenye zambi, watu waliolemewa na uovu, kizazi cha watenda mabaya, watoto wanaoishi kwa udanganyifu! Ninyi mumemwacha Yawe, mumemuzarau Mutakatifu wa Israeli, mumerudi nyuma. Niwapige wapi tena, ninyi munaoendelea kuasi? Kichwa chote kinajaa vidonda, na moyo unaumia kabisa! Tokea kwenye muguu mpaka kwenye kichwa hakuna chenye kuwa kizima; ni machubuko, alama za mapigo na vidonda vinavyovuja damu, vilivyokosa kusafishwa, kufungwa wala kutulizwa kwa mafuta. Inchi yenu imeharibiwa kabisa; miji yenu imeteketezwa kwa moto. Wageni wamebeba mazao ya inchi yenu mbele ya macho yenu, imeharibiwa kama vile Sodoma. Sayuni umeachwa kama kibanda katika shamba la mizabibu, kama kibanda cha mulinzi katika shamba la maboga, kama muji uliozungukwa kwa vita. Yawe wa majeshi asingetuachia watu wachache, tungekwisha kuwa kama watu wa Sodoma tungekuwa na hali ileile ya Gomora. Musikilize neno la Yawe, enyi watawala waovu kama wa Sodoma! Musikilize mafundisho ya Mungu wetu, enyi watu waovu kama wa Gomora! Yawe anasema hivi: Uwingi wa sadaka zenu ni kitu gani kwangu? Nimechoka na sadaka zenu za kondoo wenye kuteketezwa na mafuta ya nyama wenu wenye kunona. Sipendezwi na damu ya ngombe dume, wala ya wana-kondoo, wala ya beberu. Munapokuja mbele yangu kuniabudu, nani aliyewaambia mukanyagekanyage ndani ya viwanja vyangu? Musiniletee tena matoleo yenu yasiyokuwa na maana; ninachukizwa na sadaka yenu ya ubani. Muache kufanya sikukuu za mwandamo wa mwezi, Sabato na mikutano ya ibada; sikubali ibada zilizochanganyika na maovu. Sipendezwi na sikukuu zenu za mwandamo wa mwezi, pamoja na sikukuu zenu zingine. Zimekuwa muzigo muzito kwangu, nami nimechoka kuzivumilia. Munapoinua mikono yenu kwa kuomba, nitauficha uso wangu nisiwaone. Hata mukiomba sana sitawasikia, maana mikono yenu imejaa damu. Mujisafishe, mujitakase; muondoe matendo yenu maovu mbele yangu. Muache kutenda mabaya, mujifunze kutenda mema. Mufuate sheria ya Mungu, mumusaidie mwenye kuteswa, mumupatie yatima haki yake, mutetee haki za wajane. Yawe anasema hivi: Mukuje basi, tukate shauri. Zambi zenu zikionekana kuwa nyekundu, zitakuwa nyeupe kama teluji; zikionekana kuwa nyekundu sana, zitakuwa nyeupe kama sufu. Mukiwa tayari kunitii, mutakula mazao mema ya inchi. Lakini mukikataa na kuniasi, mutaangamizwa kwa upanga. Maneno haya yanatoka katika kinywa cha Yawe. Namna gani muji uliokuwa mwaminifu sasa umegeuka kuwa kahaba! Wakati mumoja sheria ya Mungu ilifuatwa kabisa, haki ilikaa ndani yake. Sasa, ni muji wa wauaji. Feza yako imekuwa kama takataka; divai yako imechanganyika na maji. Wakubwa wako ni waasi; wanashirikiana na wizi. Kila mumoja anapenda kituliro, na kukimbilia zawadi. Hawamupatii yatima haki yake, haki za wajane si kitu kwao. Kwa hiyo, nitawamwangia waadui zangu hasira yangu, nitawalipiza kisasi wapinzani wangu. –Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe wa majeshi, Mwenye Nguvu wa Israeli.– Nitapigana nawe; nitayeyusha uchafu wako kabisa, na kuondoa takataka yako yote. Nitakupatia waamuzi wanaokuwa sawa wale wa kwanza na washauri wanaokuwa sawa wale wa zamani. Halafu, Yerusalema utaitwa Muji wa Haki, Muji Mwaminifu. Muji Sayuni utakombolewa kwa njia ya kufuata sheria ya Mungu, nao wakaaji wake waliogeuka toka zambi zao kwa njia ya haki. Lakini waasi na wenye zambi wote wataangamizwa pamoja; wanaomwacha Yawe watateketezwa. Mutapata haya kwa ajili ya miti ya mialo muliyoipenda sana; mutafezeheka kwa sababu ya bustani mulizofurahia. Mutakuwa kama mialo ambayo majani yake yamekauka; kama shamba lisilokuwa na maji. Wenye nguvu watakuwa kama majani yenye kukauka, matendo yao yatakuwa kama cheche za moto. Watateketea pamoja na matendo yao, wala hakutakuwa mutu wa kuwaokoa. Haya ndiyo mambo Isaya mwana wa Amozi aliyofunuliwa juu ya inchi ya Yuda na Yerusalema. Katika siku zinazokuja, itatukia kwamba mulima wa nyumba ya Yawe utaimarishwa kupita milima yote, utainuliwa juu ya vilima vyote. Mataifa yote yatajaa kule, watu wengi wataenda kule na kusema, Mukuje tupandie kwenye mulima wa Yawe, tuende kwenye nyumba ya Mungu wa Yakobo, apate kutufundisha njia zake, nasi tutafuata mapito yake. Maana sheria itakuja kutoka Sayuni; neno la Yawe kutoka Yerusalema. Mungu atafanya hukumu kati ya mataifa; ataamua maneno kati ya watu wengi. Watu watafua panga za vita kuwa majembe na mikuki yao kuwa visu vya kuvuna. Taifa halitapigana na taifa lingine wala hayatafanya tena mazoezi ya vita. Sasa, enyi wazao wa Yakobo, mukuje, tutembee katika mwangaza wa Yawe. Sasa, ee Mungu, umewatupa watu wako, wazao wa Yakobo. Maana kweli wachawi kutoka mashariki wamejaa kati yao; kuna waaguzi kama vile kwa Wafilistini. Wanashirikiana na watu wageni. Inchi yao imejaa feza na zahabu, akiba yao ni kubwa zaidi. Inchi yao imejaa farasi, magari yao ya vita hayana hesabu. Inchi yao imejaa sanamu za miungu, watu wake wanaabudu kazi ya mikono yao, vitu walivyotengeneza wao wenyewe. Kwa hiyo, kila mutu atapata haya na kufezeheshwa. Usiwasamehe hata kidogo, ee Mungu! Muingie chini ya jiwe, mujifiche katika mavumbi, kwa kuepuka kitisho cha Yawe, mbali na mwangaza wa utukufu wake. Macho yenye kiburi ya wanadamu yatanyenyekezwa, watu wenye majivuno watashushwa chini, na Yawe peke yake atatukuzwa siku hiyo. Kweli, siku ya Yawe wa majeshi inakuja juu ya wote wenye kiburi na majivuno, juu ya wote wanaojitukuza, juu ya miti ya mierezi yote ya Lebanoni ambayo ni mirefu na mizuri, juu ya miti ya mialo yote katika inchi ya Basani, juu ya milima yote mirefu, juu ya vilima vyote vinavyoinuka juu sana; juu ya minara yote mirefu, juu ya kuta zote ndefu, juu ya mashua yote makubwa ya Tarsisi, na juu ya mashua yote mazuri. Kiburi cha wanadamu kitashushwa, majivuno ya watu yatanyenyekezwa, na Yawe peke yake atatukuzwa siku hiyo. Sanamu zote za miungu zitatoweka kabisa. Muingie katika mapango chini ya mawe, katika mashimo ndani ya udongo, kwa kuepuka kitisho cha Yawe, mbali na mwangaza wa utukufu wake, atakapokuja kuogopesha dunia. Siku hiyo, watu watawatupia panya na popo sanamu za feza na zahabu walizojitengenezea kusudi waziabudu. Nao wataingia katika mapango chini ya mawe na kwenye nyufa za mawe, kwa kuepuka kitisho cha Yawe, mbali na mwangaza wa utukufu wake, atakapokuja kuogopesha dunia. Usimutumainie mwanadamu, uzima wake ni kama pumzi tu. Yeye anafaa kitu gani? Sasa, Bwana wetu Yawe wa majeshi ataondoa kutoka Yerusalema na inchi ya Yuda kila tegemeo: tegemeo lote la chakula na la kinywaji. Ataondoa mashujaa na waaskari, waamuzi na manabii, waaguzi na wazee, majemadari na wakubwa, washauri, wachawi wafundi na waganga wenye maarifa. Mungu anasema: Nitaweka watoto kuwa wakubwa wao; watoto wachanga watawatawala. Watu watatesana, kila mutu na mwenzake; vijana watawazarau wazee, na watu wa ovyo ovyo watawazarau wenye heshima. Wakati huo mutu atamwambia ndugu yake wakiwa bado katika nyumba ya baba yao: Wewe uko na nguo; utakuwa mukubwa wetu. Kamata utawala juu ya mabomoko haya! Lakini siku hiyo atasema: Mimi siwezi kuwa muponyaji. Ndani ya nyumba yangu hamuna chakula wala nguo. Musinifanye mimi kuwa mukubwa wenu. Watu wa Yerusalema wamejikwaa, watu wa Yuda wameanguka, kwa sababu wanamupinga Yawe kwa maneno na matendo, wakizarau utukufu wake kati yao. Ubaguzi wao unashuhudia juu yao; wanatangaza zambi yao kama vile watu wa Sodoma, wala hawaifichi. Ole kwao watu hao, kwa sababu wamejiletea maangamizi wenyewe. Muwaambie watu wa haki jinsi wanavyokuwa na heri, maana watakula matunda ya matendo yao. Lakini ole kwao watu waovu! Mambo yatawaendekea vibaya, maana yale waliyotenda yatawapata wao wenyewe. Watu wangu watateswa na watoto; wanawake ndio watakaowatawala. Enyi watu wangu, wakubwa wenu wanawapotosha, wanavuruga njia munayopaswa kufuata. Yawe yuko tayari kuanza mashitaki, anasimama kwa kuwahukumu watu wake. Yawe anawashitaki wazee na wakubwa wa watu wake: Ninyi ndio mulioliharibu shamba la mizabibu; mali wamasikini walizonyanganywa ziko ndani ya nyumba zenu. Muna haki gani kuwagandamiza watu wangu, na kuwatendea wamasikini vibaya? –Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe wa majeshi. Yawe anasema: Wanawake wa Sayuni wako na kiburi; wanatembea wakiinua kichwa juu, wakirembua macho yao kwa tamaa. Hatua zao ni za maringo, nao wanalilisha mikufu kwenye miguu yao. Basi, mimi Yawe nitawaazibu; nitawanyoa nywele hao wanawake wa Sayuni, na kuwavua nguo za kufunika uchi wao. Siku zinakuja ambapo Yawe atawanyanganya wanawake wa Yerusalema vitu vyote wanavyoringia: pete za miguu, vitana, mibano ya nywele, pete za masikio, vikomo na vitambaa vya ushungi, vitambaa vya kichwa, mikufu, mikaba iliyosokotwa, hirizi na mikufu ya kuleta bahati, pete za vidole na pua, nguo za sikukuu, kanzu, vitambaa vya kichwa na mifuko ya mikono, nguo nzuri, shemizi nzuri, vioo na vitambaa mbalimbali. Kwa pahali pa harufu ya marasi watatoa uvundo; kwa pahali pa mikaba mizuri watatumia kamba; kwa pahali pa nywele nzuri watakuwa na upaa; kwa pahali pa nguo nzuri watavaa magunia; uzuri wao wote utageuka kuwa haya. Wanaume wenu wataangamia kwa upanga, watu wenu wenye nguvu watakufa katika vita. Halafu watu watalia na kuomboleza kwenye milango ya muji; nao wataikaa ndani ya mavumbi katika ukiwa. Wakati huo wanawake saba watashikamana na mwanaume mumoja na kumwambia: Chakula na mavazi tutajitafutia wenyewe, lakini wewe utuondolee haya yetu, uturuhusu tuitwe kwa jina lako. Siku ile, tawi Yawe atakalochipuza litakuwa zuri na tukufu, nayo matunda ya inchi yatakuwa na heshima na utukufu kwa wale Waisraeli watakaobaki. Waisraeli watakaobaki watasifiwa na kujivunia mazao ya inchi yao. Wale watakaobaki wazima katika Yerusalema, huko Sayuni, wataitwa Wachaguliwa wa Mungu; hao ndio wale wote watakaokuwa wameandikwa katika kitabu chake waishi huko Yerusalema. Bwana atawatakasa wanawake wa Sayuni toka uchafu wao na kusafisha damu iliyomwangika katika Yerusalema, kwa njia ya upepo wa hukumu na wa kuunguza. Halafu, kila pahali juu ya mulima Sayuni na juu ya mikutano ya watu atafanya kuwe wingu wakati wa muchana, na moshi na moto unaowaka vizuri wakati wa usiku. Zaidi ya hayo utukufu wa Mungu utaufunika na kuulinda muji wote. Utukufu wake utakuwa kwao kivuli kwa kuwakinga na joto la muchana; na kimbilio na kikingio chao wakati wa zoruba na mvua. Nitaimba juu ya rafiki yangu, wimbo wa rafiki yangu na shamba lake la mizabibu: Rafiki yangu alikuwa na shamba la mizabibu juu ya kilima chenye udongo muzuri. Alililima vizuri na kuondoa mawe yote, akapanda humo mizabibu bora, alijenga munara wa ulinzi katikati yake, akachimba kikamulio cha divai. Kisha akatazamia lizae zabibu nzuri. Lakini likazaa zabibu chungu. Kwa hiyo rafiki yangu anasema hivi: Enyi wakaaji wa Yerusalema na watu wa Yuda, tafazali mukuwe waamuzi kati yangu na shamba langu. Ni kitu gani nilichokosa kulifanyia shamba langu? Nilipotazamia lizae zabibu nzuri, mbona basi, likazaa zabibu chungu? Na sasa nitawaambia jinsi nitakavyolifanya hilo shamba langu. Nitaubomoa upango wake, nalo litaharibiwa. Nitaubomoa ukuta wake, nalo litakanyagwakanyagwa. Nitalifanya ukiwa kabisa, mizabibu yake haitasafishwa matawi wala kupaliliwa. Litaota michongoma na miiba. Tena nitayaamuru mawingu yasinyeshe mvua juu yake. Shamba la mizabibu la Yawe wa majeshi ni taifa la Waisraeli, na mizabibu mizuri aliyoipanda ni watu wa Yuda. Yeye alitazamia watu wafuate sheria yake, akaona mauaji; alitazamia haki, alisikia kilio! Ole kwao wanaoongeza nyumba juu ya nyumba, wanaoongeza mashamba juu ya mashamba yao, mpaka kila sehemu inakuwa mali yao, na hakuna nafasi kwa wengine katika inchi. Nimemusikia Yawe wa majeshi akisema hivi: Hakika nyumba nyingi zitabaki tupu, zile kubwa na nzuri zitabaki wazi bila wakaaji. Shamba la mizabibu lenye hektari kumi litatoa litre makumi tano tu za divai; anayepanda kilo mia moja za mbegu atavuna kilo kumi tu. Ole kwao wanaoamuka asubui mapema wapate kukimbilia kinywaji cha kulewesha; wanaokesha hata usiku, mpaka divai iwaleweshe! Katika karamu zao, hapakosekani vinubi, zeze, ngoma, filimbi na divai. Lakini hawajali matendo ya Yawe, wala kutambua kazi za mikono yake. Kwa hiyo, watu wangu watapelekwa katika uhamisho kwa sababu ya ukosefu wao wa akili. Wakubwa wao watakufa na njaa, watu wengi watakufa na kiu. Kuzimu inawangoja kwa hamu kubwa, imepanua kinywa chake mpaka mwisho. Waheshimiwa pamoja na watu wengine wa Yerusalema wanaingia humo makundi kwa makundi, vilevile na wote wanaushangilia kwa furaha. Kila mutu atafezeheshwa, na wenye kiburi wote watapatishwa haya. Lakini Yawe wa majeshi anatukuzwa wakati sheria yake inafuatwa. Utakatifu wa Mungu Mutakatifu unaonyeshwa wakati haki inatendwa. Wana-kondoo watakula majani kule, kama vile katika shamba la kuwakulishia. Wana-mbuzi wanono watatafuta chakula chao kule kule. Ole kwao wanaokokota uovu kama kwa kamba; wanaoburura zambi kama wanavyokokota gari. Wanasema: Muache Yawe afanye haraka, tunataka kuona yale aliyosema atayafanya! Mutakatifu wa Israeli atimize basi kusudi lake kusudi tuone ana mipango gani! Ole kwao wanaosema ubaya ni uzuri na uzuri ni ubaya. Wanasema giza ni mwangaza na mwangaza ni giza. Wanasema kichungu ni kitamu na kitamu ni kichungu. Ole kwao wanaojiona kuwa wenye hekima na akili. Ole kwao wanaokuwa wafundi wa kunywa divai, wanaokuwa hodari sana wa kuchanganya vinywaji vya kulewesha. Kwa ajili ya kituliro kidogo wanawaachilia wenye kosa na kuwanyima wasiokuwa na kosa haki yao. Kwa hiyo, kama vile moto unavyoteketeza nyasi, kama vile majani yanavyotoweka ndani ya moto, ndivyo mizizi yao itakavyooza, na maua yao yatakavyopeperushwa juu kama mavumbi. Maana wameacha sheria ya Yawe wa majeshi, wamezarau neno la yule Mutakatifu wa Israeli. Kwa hiyo hasira ya Yawe iliwawakia watu wake, akaunyoosha mukono wake juu yao, akawaazibu. Milima ikatetemeka, maiti zao zikakuwa kama takataka katika barabara za muji. Hata hivyo, hasira yake haijatulia, angali ananyoosha mukono wake kwa kuwaazibu. Yawe ananyunyua bendera kwa kuita taifa la mbali; anawapigia filimbi watu kutoka miisho ya dunia; nao wanakuja mbio na kufika haraka! Hawachoki wala hawajikwai; hawasinzii wala hawalali; hakuna mukaba wao uliofunguka wala kamba ya kiatu iliyokatika. Mishale yao ni mikali sana, pinde zao zimevutwa tayari. Kwato za farasi wao ni ngumu kama mawe; mwendo wa magurudumu ya magari ni kama wa upepo mukali. Waaskari wao wananguruma kama simba; wananguruma kama simba wakali ambao wamekamata nyama wao na kuwapeleka mbali ambapo hakuna anayeweza kuwanyanganya. Siku hiyo, watanguruma juu ya Israeli kama uvumi wa bahari iliyochafuka. Atakayeiangalia inchi kavu ataona giza tupu na taabu, mwangaza utafunikwa na mawingu. Katika mwaka mufalme Uzia alipokufa, nilimwona Bwana katika maono akiikaa katika kiti cha kifalme kinachoinuka juu sana. Pindo la nguo yake lilienea katika hekalu lote, na juu yake kulikuwa kumeikaa wamalaika. Kila mumoja alikuwa na mabawa sita: mawili kwa kufunika uso, mawili kwa kufunika mwili na mawili ya kuruka. Walilalamikiana mumoja kwa mwengine hivi: Mutakatifu, mutakatifu, mutakatifu ni Yawe wa majeshi! Dunia yote imejaa utukufu wake. Sauti yao iliitikisa misingi ya milango ya hekalu, nalo likajaa moshi. Basi, mimi nikasema: Ole kwangu! Mimi nimeangamia, maana, midomo yangu ni michafu, na watu ninaoishi nao ni wenye midomo michafu. Hata hivyo, kwa macho yangu mwenyewe, nimemwona Mufalme, Yawe wa majeshi. Basi, mumoja wa hao wamalaika akaruka na kunifikia, akiwa ameshika katika mukono koleo lililokuwa na kaa la moto alilolitwaa kwenye mazabahu. Naye akinigusa nalo kwenye mudomo, akasema: Kaa hili limekugusa kwenye mudomo; umeondolewa kosa lako, umesamehewa zambi yako. Kisha nikamusikia Yawe akisema: Nimutume nani? Ni nani atakayekuwa mujumbe wetu? Nami nikajibu: Niko hapa! Unitume mimi. Naye akaniambia: Kwenda kuwaambia watu hawa hivi: Mutasikiliza sana, lakini hamutaelewa; mutaangalia sana, lakini hamutaona. Kisha akaniambia: Ufanye akili za watu hawa kuwa ngumu, masikio yao yasisikie, macho yao yasione; wasipate kuona kwa macho yao, wasipate kusikia kwa masikio yao, wasipate kuelewa kwa akili zao, na kunigeukia, nao wapate kupona. Mimi nikauliza: Bwana, mpaka wakati gani? Naye akanijibu: Mpaka wakati miji itakapobaki tupu bila wakaaji, nyumba bila watu, na inchi itakapoharibiwa kabisa. Nami Yawe nitawapeleka watu mbali, na kuifanya inchi yote kuwa matongo. Hata kukibaki sehemu moja ya kumi ya watu, nao vilevile watateketezwa. Hao watakuwa kama muti wa muvinje au wa mwalo ambao shina lake limebaki kisha kukatwa. Shina hilo ni mbegu takatifu ya mwanzo mupya. Katika siku za utawala wa Ahazi mwana wa Yotamu na mujukuu wa Uzia, wa inchi ya Yuda, Resini, mufalme wa Aramu, na Peka mwana wa Remalia, mufalme wa Israeli, walienda kuushambulia Yerusalema, lakini hawakuweza kuunyanganya. Mufalme wa Yuda alipopata habari kwamba Waaramu wanashirikiana na Waisraeli, yeye pamoja na watu wote wa Yuda waliogopa na kutetemeka kama miti inayotikiswa na upepo. Yawe akamwambia Isaya: Uende pamoja na mwana wako anayeitwa Watakaobaki-Watarudi, kukutana na mufalme Ahazi. Utamukuta katika barabara pahali wafuaji wa nguo wanapofanyia kazi, mwisho wa mufereji unaoleta maji kutoka kwenye birika la juu. Umwambie akuwe macho, atulie na asiogope wala asivunjike moyo, kwa sababu ya hasira kali ya mufalme Resini wa Aramu, na ya mwana wa Remalia. Hao wawili ni kama tu moshi wa kuni zinazozimika. Waaramu na vilevile Peka pamoja na jeshi lake la Efuraimu wamefanya mupango mubaya juu yako. Wamesema: Tuende kushambulia inchi ya Yuda, tuwaogopeshe watu wake, tuitwae inchi na kumuweka mwana wa Tabeali kuwa mufalme wao. Lakini Bwana wetu Yawe anasema hivi: Jambo hilo halitatukia. Haitakuwa vile. Tena Yawe akamwambia Ahazi: Umwombe Yawe, Mungu wako, akupe kitambulisho; kikuwe ni kutoka chini kuzimu au juu mbinguni. Ahazi akajibu: Sitaomba kitambulisho! Sitaki kumujaribu Yawe. Basi, Isaya akamujibu: Musikilize basi, enyi watu wa ukoo wa Daudi! Haitoshi kuwachokesha watu hata sasa munataka kumuchokesha Mungu wangu vilevile? Basi, Bwana mwenyewe atawapa kitambulisho: bikira atapata mimba, atazaa mutoto mwanaume na kumwita jina lake “Emanueli – Mungu Yuko Pamoja Nasi”. Atakula maziwa na asali mpaka atakapojua kukataa mabaya na kuchagua mema. Maana, mbele mutoto huyo hajajua kukataa mabaya na kuchagua mema, inchi za wafalme hao wawili unaowaogopa zitakuwa ukiwa. Yawe atakuletea wewe pamoja na watu wako na jamaa yote ya kifalme siku za taabu kuliko zile zote zilizotokea tangu wakati watu wa Efuraimu walipojitenga na watu wa Yuda; ni kusema, atawaletea ninyi mufalme wa Asuria. Wakati huo, Yawe atawapigia muunzi watu wa Misri wakuje kama mainzi toka vijito vya mito Nili; na watu wa Asuria wakuje kama nyuki kutoka inchi yao. Watakuja makundi kwa makundi na kuyajaza mabonde yenye miinuko, mapango ndani ya mawe, miiba, vichaka vyote na mashamba yote ya kukulishia nyama. Wakati ule, Bwana atalipa wembe kutoka ngambo ya muto Furati, ni kusema mufalme wa Asuria. Atawanyoa vichwa vyenu, miili yenu na ndevu zenu vilevile. Wakati ule, mutu atafuga ngombe mumoja muchanga na kondoo wawili; nao watatoa maziwa kwa wingi hata aweze kula siagi. Watu watakaobaki katika inchi watakula maziwa na asali. Wakati huo, kila pahali palipokuwa mizabibu elfu moja iliyopata vikoroti vya feza elfu moja, patakuwa michongoma na miiba mitupu. Watu watakwenda kule kuwinda kwa pinde na mishale, maana inchi yote itakuwa imejaa michongoma na miiba. Nayo milima yote iliyokuwa ikilimwa itakuwa imejaa michongoma na miiba, hata hakuna mutu atakayejaribu kwenda kule. Pahali pake itakuwa tu nafasi ya kukulishia ngombe na kondoo. Yawe aliniambia hivi: Twaa ubao mukubwa, uandike juu yake maneno yanayosomeka waziwazi: “Teka haraka. Nyanganya Upesi.” Basi, nikajipatia washuhuda wawili waaminifu ambao wangenishuhudia: Kuhani Uria na Zekaria mwana wa Yeberekia. Nikalala na muke wangu ambaye vilevile ni nabii, akapata mimba, akazaa mutoto mwanaume. Yawe akaniambia: Umupe mutoto huyo jina “Teka-haraka-nyanganya-upesi.” Maana mbele mutoto huyu hajafikia umri wa kuweza kutamka neno “Baba” au “Mama”, utajiri wa muji wa Damasiki na vitu walivyonyanganya kule Samaria vitapelekwa kwa mufalme wa Asuria. Yawe alisema nami tena, akaniambia: Kwa sababu watu hawa wameyakataa maji ya Siloa yanayotiririka polepole, wakatetemeka mbele ya mufalme Resini na mufalme Peka mwana wa Remalia, basi, Bwana wao atawaletea mafuriko makubwa ya maji ya muto Furati, ni kusema mufalme wa Asuria na nguvu zake zote; yatafurika na kupita kingo zake. Utaingia ndani ya inchi ya Yuda kwa nguvu na kufurika na kupanda mpaka kwenye shingo. Utaenea juu ya inchi yako yote, ee Emanueli! Muungane, enyi watu wa mataifa, na kufezeheshwa! Musikilize, enyi inchi za mbali katika dunia! Mujiweke tayari na kufezeheshwa. Mujiweke tayari na kufezeheshwa. Mushauriane pamoja lakini itakuwa bure; mufanye mipango lakini haitawezekana, maana Mungu Yuko Pamoja Nasi. Yawe alinionya kwa nguvu nisifuate njia za watu hawa, akaniambia: Musijiunge nao katika mashauri yao mabaya, wala musiogope yale wanayoyaogopa wala kuwa na hofu. Munitambue mimi peke yangu, Yawe wa majeshi, kuwa mutakatifu. Muniogope na kuniabudu mimi peke yangu. Mimi nitakuwa kimbilio. Nitakuwa vilevile kama jiwe la kujikwaa, jiwe kubwa la kuziangusha falme za Israeli na Yuda. Nitakuwa mutego wa kuwatega na kuwanasa wakaaji wa Yerusalema. Watu wengi watajikwaa, wataanguka na kupondekana; watanaswa katika mutego huo na kukamatwa mateka. Nitalinda agizo hilo na kuchunga mafundisho hayo kati ya wafuasi wangu. Nitamungojea Yawe ambaye amejificha mbali na wazao wa Yakobo; nitamutumainia. Mimi pamoja na watoto Yawe alionipa ni kitambulisho na mufano katika Israeli kwa jina la Yawe wa majeshi anayekaa kwenye mulima Sayuni. Watu wamoja watawaambia ninyi: Muombe shauri kwa mizimu na waaguzi wanaolia kama ndege; kwa sababu ni kawaida watu kuomba shauri kwa miungu yao, na kuomba shauri kwa wafu kwa ajili ya wanaokuwa wazima. Hakika anayesema hivyo hajapata kuona mwangaza. Lakini ninyi mushike lile agizo na mafundisho ya Mungu. Watu watatangatanga katika inchi, wenye kufazaika sana na wenye njaa. Na wakiwa na njaa, watakasirika na kumulaani mufalme wao vilevile na Mungu wao. Wataangalia juu mbinguni na kuiangalia dunia, lakini wataona tu taabu, giza na mateso makubwa. Hakuna atakayeepuka giza hilo kubwa. Lakini inchi ile iliyokuwa imepatwa na huzuni haitabaki siku zote katika giza hilo kubwa. Hapo zamani Mungu alizifezehesha inchi za Zebuluni na Nafutali, lakini siku zinazokuja atafanya kuwa na utukufu kandokando ya bahari, inchi inayokuwa ngambo ya Yordani, na hata Galilaya ambamo watu wa mataifa wanaishi. Watu waliotembea katika giza wameona mwangaza mukubwa. Watu walioishi katika inchi ya giza kubwa, sasa mwangaza umewaangazia. Wewe, ee Mungu, umeongoza taifa, umezidisha furaha yake. Watu wanafurahi mbele yako wana furaha kama kwa wakati wa mavuno, kama vile wanaogawanya vitu walivyonyanganya wanavyofurahi. Maana miti mizito waliyobeba, nira walizokuwa wamefungwa, na fimbo ya wasimamizi, umezivunjavunja kama wakati wa Wamidiani. Viatu vyote vya washambulizi katika vita na nguo zote zenye kujaa damu vitateketezwa kama kuni za kuwasha moto. Maana mutoto amezaliwa kwa ajili yetu, tumepewa mutoto mwanaume. Naye atapewa mamlaka ya kutawala. Ataitwa: “Mushauri wa Ajabu”, “Mungu Mwenye Nguvu”, “Baba wa Milele”, “Mufalme wa Amani”. Utawala wake utastawi siku zote, amani ya ufalme wake haitakoma. Atakamata madaraka ya mufalme Daudi na kutawala juu ya ufalme wake; ataustawisha na kuuimarisha kwa kufuata sheria ya Mungu na kutenda kwa haki tangu sasa na hata milele. Yawe wa majeshi atafanya mambo hayo. Yawe ametoa neno juu ya Yakobo nalo litamupata Israeli. Watu wote watatambua, ukoo wote wa Efuraimu na wakaaji wa Samaria. Kwa kiburi na majivuno wanasema: Kuta za matofali zimeanguka lakini sisi tutazijenga kwa mawe yaliyochongwa! Nyumba za nguzo za mikuyu zimeharibiwa lakini pahali pake tutajenga za mierezi. Basi, Yawe atawaletea wapinzani na kuwachochea waadui zao. Waasuria kwa upande wa mashariki, Wafilistini kwa upande wa magaribi, wamepanua vinywa vyao kwa kuimeza Israeli. Hata hivyo, hasira yake haijatulia, angali ananyoosha mukono wake kwa kuwaazibu. Ingawa aliwaazibu watu, hawakumurudilia Yawe wa majeshi. Yawe atakata katika Israeli kichwa na mukia, tawi la mingazi na nyasi, kwa muda wa siku moja tu. Kichwa ni wazee na waheshimiwa, mukia ni manabii wanaofundisha uongo. Wale wanaoongoza watu hawa wamewapotosha, na hao wanaoongozwa nao wamepotoka. Kwa hiyo, Yawe hawahurumii vijana wao, hana huruma juu ya wayatima na wajane wao; maana hakuna hata mumoja anayemufuata, kila mutu anasema upumbafu. Hata hivyo, hasira yake haijatulia, angali ananyoosha mukono wake kwa kuwaazibu. Uovu unawaka kama moto unaoteketeza michongoma na miiba; unawaka kama moto katika pori, na kutoa moshi muzito unaopanda juu katika anga. Kwa kasirani ya Yawe wa majeshi inchi imechomwa moto, na watu ni kama kuni za kuuwasha. Hakuna mutu anayemuhurumia ndugu yake; wananyanganya upande mumoja na hawatosheki; wanakula upande mwingine lakini hawashibi. Kila mumoja anamushambulia mwenzake. Manase anashambulia Efuraimu, Efuraimu anashambulia Manase na wote wawili wanashambulia Yuda. Hata hivyo, hasira ya Yawe haijatulia, angali ananyoosha mukono wake kwa kuwaazibu. Ole kwao wanaotunga sheria za uovu, watu wanaopitisha sheria za kugandamiza. Wanakataa kusambisha wazaifu, wananyanganya watu wangu wamasikini haki yao. Wanateka wajane; wananyanganya wayatima mali yao. Mutafanya nini siku ya azabu, siku zoruba itakapowakujia kutoka mbali? Mutamukimbilia nani kwa kuomba musaada? Mutakwenda wapi kwa kuweka mali yenu? Hakuna! Mutajikunja tu kati ya wafungwa na kuangamia pamoja na wanaouawa katika vita. Hata hivyo, hasira yake haijatulia, angali ananyoosha mukono wake kwa kuwaazibu. Ole kwake Asuria, yeye ni kama fimbo ya hasira yangu, yeye anayeshika kiboko cha hasira yangu! Nilimutuma kuliazibu taifa ovu, nilimwamuru kuwaazibu watu niliowakasirikia, kuwanyanganya na kuteka vitu vyao, na kuwakanyaga chini kama matope katika njia. Lakini Asuria hakuwazia hivyo, yeye alikuwa na nia ingine; alikusudia kuharibu kabisa, kuangamiza mataifa mengi sana. Maana alisema: Si kweli majemadari wangu ni wafalme? Si kweli kwamba muji wa Kalno niliutendea kama vile wa Karkemisi, muji wa Hamati kama muji wa Arpadi, Samaria kama Damasiki? Nimepata kuunyoosha mukono wangu juu ya falme zenye sanamu za miungu kubwa kuliko sanamu za Yerusalema na Samaria. Basi nitashindwa kuutendea Yerusalema na sanamu zake, kama nilivyoutendea Samaria na sanamu zake? Wakati Yawe atakapomaliza kazi zake zote kwenye mulima Sayuni na katika Yerusalema, atamwazibu mufalme wa Asuria, kwa sababu ya majivuno na kiburi chake. Maana mufalme wa Asuria alisema: Kwa nguvu zangu mwenyewe nimetenda hayo, na kwa hekima yangu, maana mimi ni mwerevu! Nimeondoa mipaka kati ya mataifa, nikanyanganya akiba zao; kama ngombe dume nimewaporomosha walioikaa juu ya viti vya kifalme. Kama mutu anayenyoosha mukono kwenye chicha, ndivyo nilivyokamata mali ya mataifa; kama mutu anayeokota mayai yaliyoachwa ndani ya chicha, ndivyo nilivyoyaokota katika dunia yote. Watu wote walikuwa sawa ndege ambaye hapigi mabawa au kufungua midomo kwa kupiga kelele. Lakini Yawe anasema hivi: Shoka litaweza kujisifu mbele ya yule anayelitumia? Musumeno unaweza kujivuna mbele ya mwenye kukata nao? Ni kama kwamba vile fimbo ingeweza kumwinua anayeishika, au gongo kumwinua mwenye kuitumia! Kwa hiyo, Bwana wetu Yawe wa majeshi, atawaletea waaskari wao wanene ugonjwa wa kuwakondesha, na utukufu wao utateketezwa kama kwa moto. Mungu anayekuwa mwangaza wa Israeli atakuwa kama moto. Mutakatifu wa Israeli atakuwa ulimi wa moto ambao kwa siku moja utateketeza kila kitu, miiba yake na michongoma zake pamoja. Pori yake yenye utukufu na mashamba yake mazuri, Yawe atayaangamiza yote; itakuwa kama mutu aliyemalizika na ugonjwa. Miti itakayobaki katika pori yake itakuwa michache sana hata mutoto mudogo ataweza kuihesabu. Siku ile wazao wa Yakobo watakaobaki, ni kusema Waisraeli watakaopona hawatalitegemea tena taifa lililowaazibu, lakini watamutegemea kabisa Yawe, Mutakatifu wa Israeli. Wazao wa Yakobo wachache watakaobaki watamurudilia Mungu Mukubwa. Maana, hata kama sasa Waisraeli ni wengi kama muchanga wa bahari, ni wachache tu watakaorudi. Maangamizi yamepangwa yafanyike, nayo yatafanyika kwa haki tu. Kweli! Bwana, Yawe wa majeshi, atakamilisha kabisa katika inchi yote jambo aliloamua kutenda. Kwa hiyo, Bwana wetu Yawe wa majeshi anasema hivi: Enyi watu wangu munaokaa Sayuni, musiwaogope Waasuria ambao wanawapiga kwa fimbo, wakiinua gongo zao juu yenu kama walivyofanya Wamisri. Maana bado kidogo, nayo hasira yangu itapita na kasirani yangu itawageukia Waasuria. Yawe wa majeshi atainua fimbo yake kama vile alivyowapiga Wamidiani kwenye jiwe la Orebu. Atanyoosha fimbo yake juu ya bahari kama vile alivyowafanyia Wamisri. Wakati huo, muzigo waliowabebesha atauondoa na nira waliyowatia kwenye shingo lenu itavunjwa. Adui amepanda kutoka Rimoni, amefika katika muji wa Ayati. Amepitia kule Migoroni, mizigo yake ameiacha katika muji wa Mikimasi. Amekwisha pita kwenye kivuko. Usiku huu analala Geba. Watu wa Rama wanatetemeka kwa hofu, wakaaji wa Gibea, muji wa Sauli, wamekimbia. Enyi watu wa Galimu, mupige kelele! Enyi watu wa Laisi, mutege sikio! Enyi wenyeji wa Anatoti, mujibu! Watu wa Madimena wamekimbia, wakaaji wa Gebimu wanatafuta makimbilio. Leo hii, adui atapiga kambi kule Noba, anainua mukono wake kwa mulima Sayuni, kilima cha Yerusalema. Bwana, Yawe wa majeshi atakata matawi kwa ukali, miti mirefu itaangushwa chini, wanaokuwa juu watashushwa. Atakata vichaka vya pori kwa shoka; Lebanoni na mierezi yake yenye utukufu itaanguka. Kutatokea chipukizi katika shina la Yese, tawi litachipuka toka mizizi yake. Roho wa Yawe atakaa kwake, Roho wa hekima na maarifa, Roho wa shauri jema na nguvu, Roho wa akili na utii wa Mungu. Furaha yake itakuwa kumutii Yawe. Hatatoa hukumu kulingana na yale anayoona, wala kuamua kufuatana na yale anayosikia. Atawaamulia wamasikini kwa haki na kutetea haki za wakosefu katika inchi. Kwa neno lake dunia itaazibiwa, kwa pumzi yake waovu watauawa. Haki itakuwa kama mukaba wa kujifunga, uaminifu utakuwa kama mukaba kwenye kiuno chake. Imbwa wa pori ataishi pamoja na mwana-kondoo, chui atapumzika pamoja na mwana-mbuzi. Wana-ngombe na wana-simba watakula pamoja, na mutoto mudogo atawaongoza. Ngombe na dubu watakula pamoja, watoto wao watapumzika pamoja; na simba atakula majani kama ngombe. Mutoto muchanga atacheza kwenye shimo la nyoka, mutoto ataweza kutia mukono kwenye shimo la nyoka wa sumu. Katika mulima mutakatifu wa Mungu hakutakuwa ubaya wala uharibifu. Maana kumujua Yawe kutaenea pote katika inchi, kama vile maji yanavyojaa katika bahari. Siku ile chipukizi wa Yese atakuwa kitambulisho kwa mataifa; mataifa yatamutafuta na makao yake yatatukuka. Siku hiyo, Bwana ataunyoosha mukono wake tena kuwarudisha watu wake waliobaki kule Asuria, Misri, Patirosi, Etiopia, Elamu, Sinari, Hamati na sehemu za visanga vya bahari. Naye atasimika bendera kuwaita mataifa, kuwakusanya Waisraeli waliozarauliwa, kuwaleta pamoja watu wa Yuda waliotawanywa, na kuwarudisha toka pembe ine za dunia. Wivu wa Efuraimu juu ya Yuda utakoma, hakutakuwa tena uadui kati ya Yuda na Efuraimu. Wote pamoja watashambulia Wafilistini wanaokuwa upande wa magaribi, pamoja watawanyanganya watu wanaokaa upande wa mashariki. Watawashinda Waedomu na Wamoabu, nao Waamoni watawatii. Yawe atakausha guba ya bahari ya Misri, kwa pumzi yake inayochoma atakausha muto Furati, nao utagawanyika katika vijito saba, watu wavuke humo miguu mikavu. Tena, kutakuwa barabara kubwa toka Asuria kwa ajili ya watu wake waliobaki humo kama ilivyokuwa kwa Waisraeli wakati walipotoka katika inchi ya Misri. Siku hiyo mutasema: Ninakushukuru, ee Yawe, maana ingawa ulinikasirikia, hasira yako imetoweka, nawe umenifariji. Mungu ndiye mwenye kuniokoa, nitamutegemea yeye, wala sitaogopa; Yawe ananijalia nguvu; yeye mwenyewe ndiye anayeniokoa. Mutachota maji kwa furaha kutoka visima vya wokovu. Siku hiyo mutasema: Mumushukuru Yawe, muombe kwa jina lake. Mujulishe kwa mataifa matendo yake, mutangaze kuwa jina lake limetukuzwa. Mumwimbie Yawe sifa maana ametenda mambo makubwa; haya yajulikane katika dunia yote. Mupige vigelegele na kuimba kwa furaha, enyi wakaaji wa Sayuni, maana Mutakatifu wa Israeli ni makubwa kati yenu. Haya ni maono, ambayo nabii Isaya mwana wa Amozi, aliyofunuliwa na Mungu juu ya inchi ya Babeli: Mungu anasema: Musimike bendera juu ya mulima usiokuwa na miti, muwapigie waaskari kelele, muwapepee watu kwa mukono, mukiwaita waingie kwenye milango ya muji wa wakubwa. Mimi nimewaamuru wachaguliwa wangu, nimewaita mashujaa wangu, hao wenye kunitukuza wakishangilia, wakuje kutimiza hasira yangu. Musikilize kelele kwenye milima kama za kundi kubwa la watu! Musikilize kelele za falme, na mataifa yanayokusanyika! Yawe wa majeshi analichunguza kundi linalokwenda kwa vita. Wanakuja kutoka inchi za mbali, wanatoka hata miisho ya dunia: Yawe na silaha za hasira yake anakuja kuiangamiza dunia. Mulie, maana siku ya Yawe imekaribia; inakuja kama uharibifu kutoka kwa Mungu Mwenye Nguvu. Kwa hiyo mikono ya kila mutu itaregea, kila mutu atavunjika moyo. Watu watafazaika, watashikwa na hofu na maumivu, watakuwa na uchungu kama mama anapozaa. Wataangalia kwa mashaka, nyuso zao zitaungua kwa haya. Siku ya Yawe inakuja, siku kali, ya kasirani na hasira kali. Itaifanya inchi kuwa uharibifu, itawaangamiza wenye zambi ndani yake. Nyota na vikundi vyake katika anga hazitaangaza; jua linapochomoza litakuwa giza, na mwezi hautatoa mwangaza wake. Yawe anasema hivi: Nitauazibu ulimwengu kwa uovu wake, waovu kwa sababu ya makosa yao. Nitakikomesha kiburi cha wenye majivuno, na kuporomosha mazarau ya watu wakali. Nitawafanya watu kuwa wachache kuliko zahabu safi; wanadamu watakuwa wachache kuliko zahabu ya Ofiri. Nitazitetemesha mbingu nayo inchi itatikisika katika misingi yake kwa sababu ya kasirani ya Yawe wa majeshi, siku ile ya hasira yangu kali. Kama swala anayewindwa, kama kondoo wasiokuwa na muchungaji, kila mumoja atajiunga na watu wake, kila mutu atakimbilia katika inchi yake. Yeyote atakayeonekana atapigwa mukuki, atakayekamatwa atauawa kwa upanga. Watoto wao wachanga watapondwapondwa mbele yao, watanyanganywa nyumba zao, na watalala na wake zao kwa kinguvu. Ninawachochea Wamedi juu yao; watu ambao hawajali feza wala hawavutwi na zahabu. Mishale yao itawaua vijana, hawatarehemu watoto, wala kuwahurumia watoto wachanga. Babeli ni utukufu wa falme zote na sifa na majivuno ya Wakaldea utakuwa kama Sodoma na Gomora, wakati Mungu alipoiangamiza. Hautakaliwa tena na watu hata kidogo, watu hawataishi humo katika vizazi vyote. Hakuna Mwarabu atakayesimamisha hema yake humo, wala muchungaji atakayechunga nyama wake humo. Pahali pake ni nyama wakali wa pori ndio watakuwa ndani yake, bundi watajaa katika nyumba zake. Mbuni wataishi humo, pepo watachezea huko. Fisi watalia ndani ya pango zake, mbweha wataonekana ndani ya nyumba zao za raha. Wakati wa Babeli umekaribia, wala siku zake hazitaongezwa. Yawe atawahurumia tena watu wa Yakobo, atawachagua tena Waisraeli. Atawarudisha katika inchi yao wenyewe, na wageni watakuja na kukaa pamoja na watu wa Yakobo. Watu wa mataifa watawasaidia Waisraeli kurudi katika inchi waliyopewa na Yawe. Na hapo watawatumikia Waisraeli kama watumwa. Wale waliowateka sasa watatekwa na Waisraeli, na watawatawala wale waliowatesa. Ewe Israeli, wakati Yawe atakapokufariji nyuma ya mateso, mahangaiko na utumwa uliofanyiwa, utaimba wimbo huu wa kumuchekelea mufalme wa Babeli: Jinsi gani mutesaji alikomeshwa! Ukali wake umekomeshwa! Yawe amelivunja gongo la waovu, ameivunja fimbo ya kifalme ya watawala, ambayo walipiga nayo watu kwa hasira bila kukoma, na kuwatawala kwa kuwatesa bila huruma. Sasa dunia yote ina utulivu na amani, kila mutu anaimba kwa furaha. Miti ya shindano inafurahia kuanguka kwako, nayo mierezi ya Lebanoni pamoja inasema: Kwa vile sasa umeangushwa, hakuna mukata miti atakayekuja juu yetu! Kuzimu nako kumechangamuka, kusudi ya kukupokea wakati utakapokuja. Kunaiamusha mizimu ikuje kukusalimia na wote waliokuwa wakubwa wa dunia; kunawasimamisha kutoka kwenye viti vyao vya kifalme wote waliokuwa wafalme wa mataifa. Wote kwa pamoja watakuambia: Nawe sasa umekuwa zaifu kama sisi! Umekuwa kama sisi wenyewe! Utukufu wako umeteremushwa kuzimu pamoja na muziki wa vinubi vyako. Chini mafunza ndio kitanda chako, na wadudu ndio blanketi yako! Jinsi gani ulivyoporomoshwa toka mbinguni, wewe uliyekuwa nyota yenye kuangaza kwa mapambazuko. Jinsi gani ulivyoangushwa chini, wewe uliyeyashinda mataifa! Wewe ulijisemesha ndani ya moyo wako: Nitapanda mpaka mbinguni; nitaweka kiti changu juu ya nyota za Mungu, nitaikaa juu ya mulima pahali miungu wanapokutana, huko mbali pande za kaskazini. Nitapanda juu ya mawingu nitajifanya kuwa sawa na Mungu Mukubwa. Lakini umeporomoshwa mpaka kuzimu; umeshushwa chini kabisa ndani ya shimo. Watakaokuona watakutonolea macho, watakushangaa wakisema: Huyu ndiye aliyetetemesha dunia na kuzitikisa falme, aliyegeuza dunia kuwa kama jangwa, akaangamiza miji yake, na kukataa kuwafungua wafungwa wake? Wafalme wote wa mataifa wamezikwa kwa heshima kila mumoja ndani ya kaburi lake. Lakini wewe umetupwa inje ya kaburi lako, kama mutoto wa kuchukiza aliyezaliwa mufu, kama maiti ambayo imekanyagwakanyagwa. Umelundikiwa maiti za waliouawa kwa upanga, waliotupwa ndani ya mashimo penye mawe. Lakini wewe hautaunganishwa nao katika mazishi, maana uliiharibu inchi yako, uliwaua watu wako. Wazao wa waovu wasahauliwe kabisa! Mujitayarishe kuwachinja watoto wake kwa sababu ya makosa ya baba zao, wasipate kuamuka na kukamata inchi, na kuijaza dunia yote miji yao. Nitaushambulia muji wa Babeli na kuuangamiza kabisa. –Ni ujumbe wa Yawe wa majeshi.– Nitaharibu kila kitu, muji wote, watoto na yeyote aliyebaki muzima. –Ni ujumbe wa Yawe.– Nitaufanya kuwa makao ya nungunungu, na utakuwa tingitingi ya maji. Nami nitaufagilia mbali kwa ufagio wa maangamizi. –Ni ujumbe wa Yawe wa majeshi. Yawe wa majeshi ameapa: Kama nilivyopanga, ndivyo itakavyokuwa; kama nilivyokusudia, ndivyo itakavyokamilika. Nitauvunja uwezo wa Waasuria katika inchi yangu; nitawakanyagakanyaga katika milima yangu. Nitawaondolea watu wangu nira yao ya unyanganyi, na muzigo wa mateso yao. Huu ndio uamuzi wa Yawe juu ya dunia yote; hii ndiyo azabu atakayotoa juu ya mataifa yote. Kama Yawe wa majeshi ameamua, nani atakayeweza kuvunja uamuzi wake? Kama anaunyoosha mukono wake kutoa azabu, ni nani atakayemupinga? Mwaka mufalme Ahazi alipokufa, Mungu alitoa ujumbe huu: Musishangilie, enyi Wafilistini wote, kwamba Asuria, fimbo iliyowapiga, imevunjika; maana, nyoka wa kawaida atazaa nyoka mwenye sumu, na nyoka mwenye sumu atazaa nyoka mukubwa mwenye kuruka. Wazaliwa wa kwanza wa wazaifu watashiba, na wakosefu watakaa kwa usalama. Lakini chipukizi wenu nitawaua kwa njaa; na yeyote kati yenu atakayebaki nitamwua. Ulie ewe mulango; ulalamike ewe muji; tetemeka kwa hofu, ewe inchi yote ya Filistia. Maana moshi wa waaskari unakuja kutoka kaskazini, wala hakuna atakayechelewa katika makundi yake. Basi watapewa jibu gani wajumbe wa taifa hilo? Wataambiwa: Yawe ameijenga imara Sayuni, na wamasikini kati ya watu wake watakimbilia kule. Ujumbe wa Mungu juu ya inchi ya Moabu. Muji wa Ari katika inchi ya Moabu umeangamizwa usiku; muji wa Kiri katika inchi ya Moabu umeangamizwa usiku. Watu wa Diboni wamepanda katika hekalu pahali pa juu kwa kuomboleza, watu wa Moabu wanalia kwa ajili ya Nebo na Medeba; vichwa vyote vimenyolewa upaa, ndevu zao zote zimekatwa kabisa. Wanapita katika njia wakivaa magunia. Kwenye paa za nyumba na viwanja vya muji watu wanalia na kukauka kwa machozi. Watu wa Hesiboni na Eleale wanalia, sauti zao zinasikilika mpaka Yasa. Hata waaskari wa Moabu wanalia kwa sauti; mioyo yao inatetemeka. Moyo wangu unaugua kwa ajili ya inchi ya Moabu; wakimbizi wake wanakimbilia Zoari, wanakimbia mpaka Egilati-Selisiya. Wanapanda njia ya kwenda Luhiti wakilia, katika njia kwenda Horonaimu wanatoa kilio cha maangamizi. Kijito cha Nimurimu kimekauka; nyasi zimekauka, majani mabichi yamenyauka, hakuna chochote kinachoota hapo. Wakimbizi wanavuka kijito cha Mierebi; wamebeba mali yao yote waliyopata, na kila kitu walichojiwekea kama akiba. Kilio kimesikilika pote katika inchi ya Moabu, maombolezo yao yamefika Eglaimu, yamefika hata mpaka Beri-Elimu. Maji ya Dimoni yamejaa damu, lakini Mungu ataongeza musiba wa Dimoni. Hao wachache watakaobaki wazima na kukimbia kutoka Moabu, watapelekewa simba wa kuwaua. Mupeleke wana-kondoo kwa mutawala wa inchi, mupeleke kutoka Sela katika jangwa mpaka kwenye mulima Sayuni. Kama ndege wanavyohangaika na kurukaruka, wakiwa wamefukuzwa kutoka chicha zao, ndivyo wabinti wa Moabu wanavyokuwa kwenye vivuko vya Arnoni. Wamoabu wanawaambia watu wa Yuda: Mutuongoze, mutuamue. Mueneze ulinzi wenu juu yetu, kama vile usiku unavyoeneza kivuli chake. Mutufiche sisi wakimbizi; musitutoe sisi tuliofukuzwa. Wakimbizi wa Moabu waishi kwenu, mukuwe kimbilio lao mbali na mwangamizaji. Mutesaji atakapokuwa ametoweka, mateso yatakapokuwa yamekoma, na wagandamizaji kutoweka katika inchi. Kisha utawala wa wema utazinduliwa katika hema ya Daudi. Mutawala atakuwa mwaminifu. Atahukumu kufuatana na sheria ya Mungu, atakuwa mwepesi wa kutenda kwa haki. Watu wa Yuda wanasema hivi: Tumesikia juu ya kiburi cha Moabu, tunajua jinsi alivyojivuna sana; tumesikia juu ya majivuno, kiburi na mazarau yake; lakini majivuno yake hayo ni bure. Sasa Wamoabu wanalia; wote wanaomboleza juu ya inchi yao. Muomboleze kwa ajili ya pigo hilo kubwa, na juu ya maandazi ya zabibu za Kiri-Hareseti. Mashamba ya Hesiboni yamefifia, vilevile na zabibu za Sibuma ambazo ziliwalewesha wakubwa wa mataifa. Zikafika Yaweri na kusambaa hata katika jangwa, chipukizi zake zikafika hata ngambo ya bahari. Kwa hiyo ninalia pamoja na Yaweri kwa ajili ya mizabibu ya Sibuma. Machozi yananitoka kwa ajili yenu, enyi miji ya Hesiboni na Eleale; maana vigelegele vya mavuno ya matunda na ya ngano vimetoweka. Furaha na shangwe zimetoweka katika shamba lenyi mavuno mengi. Kwenye mizabibu hakuna kuimba tena, wala kupiga vigelegele. Hakuna tena kukamua zabibu ndani ya vikamulio, sauti za furaha za mavuno zimekomeshwa. Hivyo, nafsi yangu inalilia Moabu kama kinubi, na moyo wangu kwa ajili ya muji wa Kiri-Heresi. Watu wa Moabu wanapojitokeza kuabudu mungu wao, wanapojichokesha huko juu pahali pa ibada, wanapokwenda pahali pao patakatifu kwa kuomba, hawatakubaliwa. Hili ndilo jambo Yawe alilosema wakati uliopita juu ya Moabu. Lakini sasa Yawe anasema hivi: Nyuma ya miaka mitatu kamili, ikihesabiwa kama vile mutumishi anavyohesabu siku zake, utukufu wa Moabu utapunguka. Ingawa watu wake ni wengi, watakaobaki wazima watakuwa wachache na wazaifu. Ujumbe wa Mungu juu ya muji wa Damasiki. Damasiki utakoma kuwa muji; utakuwa lundo la mabomoko. Miji inayokuwa chini yake imeachwa matongo milele. Itakuwa makao ya makundi ya nyama, wala hakuna mutu atakayewatisha. Pango za Efuraimu zitatoweka, na utawala wa Damasiki utakwisha. Waaramu ambao watabaki wazima, hawatakuwa na utukufu zaidi kama wazao wa Israeli. –Ni ujumbe wa Yawe wa majeshi. Siku hiyo, utukufu wa Yakobo utaporomoshwa, na unono wake utapotea. Itakuwa kama wakati wa mavuno, wakati wamekwisha kuokota ngano, na kukusanya masuke katika mukono. Hakika, itakuwa kama bonde la Refaimu wakati wamekwisha kuvuna ngano. Watabaki wachache kama vile kisha kuangusha matunda ya mizeituni: matunda mawili au matatu katika tawi la juu; mane, matano katika matawi yanayozaa sana. –Ni ujumbe wa Yawe, Mungu wa Israeli. Siku hiyo, watu watamwangalia Muumba wao, na kuelekeza macho yao kwa huyo Mutakatifu wa Israeli. Hawataelekea tena mazabahu ambazo ni kazi za vidole vyao wenyewe, wala kuzitazamia tena kazi za mikono yao wenyewe, ni kusema sanamu za mungu Ashera na mazabahu za kufukizia ubani. Siku hiyo miji yao imara itaachwa matongo, kama miji ambayo Wahivi na Waamori waliihama walipokuwa wakiwakimbia wazao wa Israeli. Kila kitu kitakuwa uharibifu. Maana wewe Israeli umemusahau Mungu aliyekuokoa, haukukumbuka Jiwe lako la kufichamia. Kwa hiyo, hata mukipanda mimea ya Bali, na kuitakasa kwa mungu wa kigeni; hata mukiifanya ikomae siku hiyohiyo muliyoipanda na kuifanya ichanue asubui hiyohiyo, mavuno yenu yatatoweka siku hiyo ya hasara na maumivu yasiyoweza kuponyeshwa. Aha! Ngurumo ya watu wengi! Wananguruma kama bahari. Aha! Mulio wa watu wa mataifa! Yanatoa mulio kama wa maji mengi. Mataifa yananguruma kama ngurumo ya maji mengi, lakini Mungu atayakaripia, nayo yatakimbilia mbali. Yatafukuzwa kama maganda juu ya mulima mbele ya upepo; kama mavumbi yanayonyanyuliwa na upepo mukali. Wakati wa magaribi yanaleta hofu kubwa, lakini mbele ya asubui yametoweka! Ndilo litakalowapata wale wanaotukamata na kutunyanganya mali yetu. Ole, kwa inchi iliyojaa muvumo wa mabawa, inchi inayokuwa ngambo ya mito ya Kushi! Inatuma wajumbe ambao wanasafiri ndani ya muto Nili, wamepanda ndani ya mitumbwi iliyotengenezwa na matete. Muende, enyi wajumbe wepesi, kwa taifa kubwa na hodari, la watu warefu wenye ngozi laini, wanaotisha kwa karibu na kwa mbali, taifa la watu wenye nguvu na ushindi, ambalo inchi yake imegawanywa na mito. Enyi wakaaji wote katika ulimwengu, nanyi munaojaza dunia! Bendera itakaposimikwa kwenye mulima, muangalie! Baragumu itakapopigwa, musikilize. Maana, Yawe ameniambia hivi: Tokea juu kwenye makao yangu nitaangalia yanayotukia, nikitulia kama joto katika mwangaza wa jua, kama wingu la umande wakati wa mavuno. Maana, mbele ya mavuno, wakati wa kuchanua umekwisha, maua yameanguka na kuwa zabibu yenye kukomaa, Mungu atakata chipukizi kwa upanga, na kuyakwanyua matawi. Yote yataachiwa ndege wa milima na nyama wengine wa pori. Ndege wakali watakaa humo wakati wa jua, na nyama wa pori watafanya makao humo wakati wa baridi. Wakati huo, Yawe wa majeshi ataletewa sadaka kutoka kwa watu warefu na wenye ngozi laini, watu wanaotisha kwa karibu na kwa mbali, taifa la watu wenye nguvu na ushindi, ambalo inchi yake imegawanywa na mito. Ataletewa sadaka hizo kwenye mulima Sayuni anapoabudiwa yeye Yawe wa majeshi. Ujumbe wa Mungu juu ya inchi ya Misri. Yawe amepanda juu ya wingu linaloenda mbio na kuja mpaka katika inchi ya Misri. Sanamu za miungu ya Wamisri zitatetemeka mbele yake, mioyo ya Wamisri itayeyuka kwa woga. Mimi nitawachonganisha Wamisri wao kwa wao. Ndugu atapigana na ndugu yake, jirani atapigana na jirani yake, muji mumoja na muji mwingine, mufalme mumoja na mufalme mwingine. Nitawaondolea Wamisri uhodari wao. Nitaivuruga mipango yao. Watatafuta shauri kwa sanamu na mizimu, wachawi, mizuka na pepo. Nitawatia Wamisri katika mikono ya bwana mukali, mufalme mukali ambaye atawatawala. –Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe wa majeshi. Maji ya muto Nili yatakaushwa, nao utakauka kabisa. Mifereji yake itatoa harufu mbaya, vijito vyake vitapunguka na kukauka. Nyasi na matete yake yataoza. Sehemu za kandokando ya Nili zitakuwa tupu. Mimea yote iliyopandwa humo itakauka na kupeperushiwa mbali na kutoweka. Wavuvi wataomboleza, wote wanaotumia ndoana watalalamika, wote wanaotega nyavu humo watavunjika moyo. Wafuma nguo za kitani watafazaika, wote kwa pamoja watavunjika moyo. Wafuma nguo watafezeheshwa, na wafanya kazi watahuzunika. Wakubwa wa muji wa Soani ni wapumbafu kabisa, washauri wa Mufalme wa Misri wanatoa shauri la kijinga! Kila mumoja anaweza namna gani kumwambia Mufalme wa Misri: Mimi ni wa uzao wa wenye hekima, wa uzao wa wafalme wa zamani! Wako wapi, ewe Mufalme wa Misri, wenye hekima wako? Uwaache basi wakwambie na kukujulisha mambo Yawe wa majeshi aliyopanga juu ya Misri! Lakini wakubwa wa Soani ni wapumbafu, wakubwa wa Nofi wamedanganyika. Hao wanaokuwa musingi wa makabila yao wamelipotosha taifa la Misri. Yawe amewamwangia roho ya fujo, wakawapotosha Wamisri katika mipango yao yote, nao wakakuwa kama mulevi anayeyumbayumba akitapika. Hakuna mutu yeyote katika inchi ya Misri, mutawala au wanainchi, wakubwa au watu wadogo, anayeweza kufanya jambo lolote la maana. Siku ile watu wa Misri wataogopa kama wanawake. Watatetemeka kwa hofu watakapomwona Yawe wa majeshi ameunyoosha mukono wake juu yao. Yuda atakuwa kitisho kikubwa kwa Wamisri. Wote watakaoambiwa habari za Yuda wataingiwa na woga kwa sababu ya jambo Yawe wa majeshi aliloamua kuwatendea. Siku hiyo luga ya Kiebrania itatumika katika miji mitano ya Misri, na watu wa miji hiyo wataapa kuwa waaminifu kwa Yawe wa majeshi. Muji mumoja kati ya miji hiyo utaitwa “Muji wa Jua”. Siku hiyo, kutakuwa mazabahu kwa ajili ya Yawe katikati ya inchi ya Misri, na nguzo iliyotakaswa kwa ajili ya Mungu kwenye mpaka wa Misri. Mazabahu hayo yatakuwa kitambulisho na ushuhuda kwa Yawe wa majeshi katika inchi ya Misri. Watu wakimulilia Yawe humo kwa sababu ya kugandamizwa, yeye atawapelekea mukombozi atakayewatetea na kuwakomboa. Yawe atajijulisha kwa Wamisri na hapo ndipo Wamisri watakapomwitikia na kumwabudu kwa kumutolea matoleo na sadaka za kuteketezwa. Vilevile watafanyia Yawe viapo ambavyo watavitimiza. Yawe atawaazibu Wamisri na kuwaponya. Nao watamurudilia, naye atayasikiliza maombi yao na kuwaponya. Wakati huo, kutakuwa barabara kubwa kutoka inchi ya Misri mpaka katika inchi ya Asuria. Waasuria watawatembelea Wamisri, na Wamisri watawatembelea Waasuria; nao wote watamwabudu Mungu pamoja. Wakati huo, Israeli itahesabiwa pamoja na Misri na Asuria; mataifa haya matatu yatakuwa baraka kwa dunia yote. Yawe wa majeshi atawabariki na kusema: Wabarikiwe Wamisri watu wangu, vilevile na Waasuria ambao ni kitambulisho cha kazi yangu na Waisraeli wanaokuwa urizi wangu. Sargoni, mufalme wa Asuria, alimutuma jemadari wake mukubwa kushambulia muji wa Asidodi. Naye akaushambulia na kuuteka. Miaka mitatu mbele ya pale, Yawe alimwambia Isaya mwana wa Amozi hivi: Kwenda uvue nguo ya gunia uliyokuwa umevaa katika kiuno, na viatu vyako. Isaya akafanya kama alivyoambiwa; akakuwa anatembea uchi na bila viatu. Yawe akasema: Mutumishi wangu Isaya amekuwa akitembea uchi na bila viatu kwa muda wa miaka mitatu sasa, kama kitambulisho juu ya inchi za Misri na Kushi. Basi, mufalme wa Asuria atawapeleka Wamisri na Wakushi kuwa wafungwa, wakubwa kama vile wadogo. Watapelekwa, nao watatembea uchi na bila viatu, matako wazi. Misri ipate haya! Kisha wote waliotegemea Kushi na kujivunia Misri watajuta na kufazaika. Wakati huo, wakaaji wa kandokando watasema: Muangalie yaliyowapata watu tuliowategemea na kuwakimbilia kuomba musaada watuokoe na mufalme wa Asuria! Na sasa, sisi tutaweza namna gani kupona? Ujumbe wa Mungu juu ya jangwa kando ya bahari. Kama upepo mukali unaovuma kutoka kusini, washambulizi wanakuja kutokea katika jangwa, kutoka katika inchi ya kutisha. Nimeonyeshwa maono ya kutisha: wadanganyifu wanadanganya na waangamizaji wanaangamiza. Mupande kwa kupigana vita, enyi Waelamu! Mushambulie, enyi Wamedi! Mungu atakomesha mateso yote yaliyoletwa na Babeli. Kwa maono hayo nimeingiwa na woga mukubwa. Maumivu mengi yamenishika, kama maumivu ya mama anayezaa. Nimefazaika zaidi hata siwezi kusikia; nimefazaika hata siwezi kuona. Moyo unanidunda na woga umenishika. Nilitamani magaribi ifike, lakini ilipofika ikakuwa ya kutetemesha. Chakula kimetayarishwa, mikeka zimetandikwa, sasa watu wanakula na kunywa. Kwa rafla, sauti inasikilika: Musimame enyi watawala! Muweke silaha tayari! Bwana aliniambia: Kwenda uweke mulinzi; umwambie atangaze atakachoona. Akiona kikundi, waaskari wapanda-farasi wawiliwawili, wapanda-ngamia na wapanda-punda, akuwe macho. Akuwe macho kabisa! Kisha, huyo mulinzi akalalamika: Bwana, nimesimama juu ya munara wa ulinzi muchana kutwa, nimeshika zamu usiku kucha! Angalia, wanakuja: waaskari wapanda-farasi wawiliwawili. Wanasema: Babeli umeanguka! Umeanguka! Sanamu zote za miungu yake zimetupwa chini na kuvunjwavunjwa! Ewe Israeli, watu wangu, enyi muliotwangwa na kupepetwa kama ngano. Sasa nimewaambia ninyi mambo niliyoyasikia kwa Yawe wa majeshi, Mungu wa Israeli. Ujumbe wa Mungu juu ya Duma. Ninasikia mutu ananiita kutoka Seiri: Mulinzi, nini kipya leo usiku? Kuna kipya chochote leo usiku? Nami mulinzi nikajibu: Asubui inakuja, vilevile usiku; ukitaka kuuliza, uliza tu; kwenda urudi tena. Ujumbe wa Mungu juu ya Arabia. Enyi makundi ya wasafiri ya Dedani, mupige kambi leo usiku katika pori za Arabia. Enyi wakaaji wa inchi ya Tema, muwape maji hao wenye kiu; muwapelekee chakula hao wakimbizi. Maana wamekimbia mapanga, mapanga yaliyochomolewa, pinde zilizovutwa na ukali wa mapigano. Maana Bwana aliniambia hivi: Katika muda wa mwaka mumoja, bila kuzidi wala kupunguka, utukufu wote wa Kedari utakwisha. Wapigapinde wachache kati ya mashujaa wa watu wa Kedari ndio watakaobaki. Ni Yawe, Mungu wa Israeli, anayesema hivyo. Ujumbe wa Mungu juu ya Bonde la Maono. Kuna nini, ee Yerusalema? Mbona watu wote mumepanda juu ya nyumba? Kwa nini munapiga kelele za shangwe, na muji wote umechangamuka na kujaa vigelegele? Watu wenu waliokufa hawakuuawa katika vita, wala hawakuuawa katika mapigano. Wakubwa wenu wote walikimbia, wakakamatwa hata mbele ya kufyatua mushale mumoja. Watu wako wote waliopatikana walitekwa, ingawa walikuwa wamekimbilia mbali. Ndiyo maana ninawaambia ninyi: musijali chochote juu yangu, muniache nilie machozi ya uchungu. Musijisumbue kunifariji kwa ajili ya kuangamizwa kwa watu wangu. Maana leo Yawe wa majeshi ametuletea fujo, kushindwa na wasiwasi katika Bonde la Maono. Kuta za muji zimebomolewa. Kilio cha wakaaji wake kinasikilika mpaka kwenye milima. Majeshi ya Elamu, pinde na mishale katika mikono, walikuja wamepanda farasi na magari ya vita; nalo jeshi la Kiri lilitayarisha ngao zake. Mabonde yako mazuri, ewe Yerusalema, yalijaa magari ya vita na farasi; wapanda-farasi walijipanga tayari kwenye milango yako. Ulinzi wote wa Yuda uliporomoka. Siku hiyo mulikwenda kutafuta silaha zilizokuwa zimelindwa katika Nyumba ya Pori, mukaona kwamba nyufa za kuta za muji wa Daudi ni nyingi, mukajaza maji ndani ya birika la chini. Mulizikagua nyumba za Yerusalema, mukazibomoa kwa kupata mawe ya kukaza kuta za muji. Katikati ya kuta hizo mulijijengea birika la kulinda maji yanapotiririka kutoka birika la zamani. Lakini hamukumutafuta Mungu aliyepanga mambo haya yote; hamukumujali yeye aliyepanga hayo yote tangu zamani. Siku hiyo, Yawe wa majeshi alitaka mulie na kuomboleza, munyoe nywele na kuvaa nguo za gunia. Lakini ninyi mukafurahi na kusherehekea. Mulichinja ngombe na kondoo, mukakula nyama na kunywa divai. Ninyi mulisema: Acha tukule na kunywa maana kesho tutakufa. Yawe wa majeshi alinifunulia haya akisema: Hakika uovu huu hautasahauliwa mbele ya kufa kwenu. Ni Yawe wa majeshi anayesema hivyo. Bwana wetu Yawe wa majeshi aliniambia niende kwa Sebuna, musimamizi wa jamaa ya kifalme, nimwambie hivi: Una haki gani kuwa huku? Una ndugu yeyote hapa, hata ukajichongea kaburi ndani ya jiwe juu ya mulima? Wewe bwana, Yawe atakutupilia mbali kwa nguvu. Atakubana kabisa na kukuzungushazungusha, kisha atakutupa kama mupira mpaka katika inchi pana. Huko utakufia karibu na magari yako ya vita unayojivunia, wewe unayezaraulisha nyumba ya bwana wako. Yawe atakuongoa toka katika madaraka yako na kukuporomosha kutoka pahali unapokuwa. Siku hiyo, nitamuleta mutumishi wangu Eliakimu mwana wa Hilkia. Nitamuvalisha nguo yako ya heshima, na mukaba wako na kumupa madaraka yako. Yeye atakuwa baba kwa watu wa Yerusalema na kwa ukoo wa Yuda. Nitaweka juu ya bega lake ufunguo wa ukoo wa Daudi. Akifungua, hakuna atakayeweza kufunga na akifunga, hakuna atakayeweza kufungua. Nitamwimarisha Eliakimu kama musumari uliopigiliwa pahali pagumu, naye atapata heshima tukufu katika ukoo wa wazee wake. Watu wote na jamaa yake, wadogo kwa wakubwa watajitegemeza kwake kama chungu na vikombe vilivyotundikwa kwenye musumari. Lakini siku moja, –Ni ujumbe wa Yawe wa majeshi– ule musumari uliopigiliwa pahali pagumu utaregea kwa uzito. Utakatwa na kuanguka. Yawe amesema. Ujumbe wa Mungu juu ya Tiro. Muomboleze, enyi mashua makubwa za kutoka Tarsisi. Kivuko na muji wenu vimeharibiwa. Mutapokea habari hizo mutakaporudia kutoka Kipuro. Munyamaze kwa mushangao, enyi wakaaji wa visanga, mutulie enyi wachuuzi wa Sidona. Wajumbe wenu walipita katika bahari kubwakubwa, walisafiri katika bahari nyingi. Mapato yenu yalikuwa ngano ya Misri, mukaweza kufanya biashara na mataifa. Umefezeheka, ewe Sidona, muji wenye upango kandokando ya bahari! Bahari yenyewe inatangaza: Sijapata kuwa na uchungu wa kuzaa, wala sijazaa; sikulea vijana wanaume, wala kukomalisha wabinti! Habari zitakapoifikia Misri kwamba Tiro imeangamizwa, Wamisri watafazaika sana. Muomboleze enyi wenyeji wa Foinike! Mujaribu kukimbilia Tarsisi. Basi, huu ndio muji wa furaha wa Tiro, muji ambao ulijengwa zamani za kale, ambao wakaaji wake walikwenda kurizi inchi za mbali? Ni nani aliyepanga mambo haya juu ya Tiro, muji uliosimika wafalme, wachuuzi wake walikuwa wakubwa, wakaheshimiwa katika dunia yote? Ni Yawe wa majeshi! Yeye ndiye aliyeyapanga haya yote. Alifanya hivyo akiharibu kiburi chao na kuwapatisha haya waheshimiwa wake. Mulime sasa udongo wenu, enyi wakaaji wa Tarsisi; maana hamuna tena kivuko kwa ajili ya mashua kubwa. Yawe ameunyoosha mukono wake juu ya bahari amezitetemesha falme; ametoa amri kuharibu makimbilio ya Kanana. Alisema: Ewe binti Sidona, hautaweza kufanya sherehe tena; hata ukikimbilia Kipuro, kule nako hautapata pumziko! (Ni Wakaldea, wala si Waasuria, waliowaacha nyama wa pori waushambulie muji wa Tiro. Wao ndio waliouzungushia muji huo minara ya kuushambulia, wakabomoa nyumba zake na kuufanya mabomoko.) Mulie enyi mashua za Tarsisi, maana kimbilio lenu limeharibiwa. Hapo muji wa Tiro utasahauliwa kwa muda wa miaka makumi saba, muda wa maisha ya mufalme. Kisha miaka hiyo makumi saba, muji wa Tiro utapatwa na kile watu wanachoimba juu ya kahaba: Kamata kinubi chako uzungukezunguke ndani ya muji, ewe kahaba uliyesahauliwa! Imba nyimbo tamutamu. Imba nyimbo nyinginyingi, kusudi upate kukumbukwa tena. Kisha miaka hiyo makumi saba, Yawe atauazibu muji wa Tiro, nao utarudia kufanya uzinzi kwa kujiuzisha kwa mataifa yote ya dunia. Feza utakayopata itatakaswa kwa ajili ya Yawe. Hawatalinda feza hiyo lakini wale wanaomwabudu Yawe wataitumia kwa kununua chakula kingi na nguo nzuri. Sasa Yawe anaiharibu dunia na kuifanya tupu. Atavuruga uso wa dunia na kuwatawanya wakaaji wake. Kila mutu atapatwa na mambo yaleyale: mutu wa kawaida na kuhani; mutumwa na bwana wake; mujakazi na bibi wake; mwenye kununua na mwenye kuuzisha; mukopeshaji na mukopaji; mwenye kudai na mwenye kudaiwa. Dunia itaharibiwa kabisa na kuangamizwa. Ni Yawe amesema hayo. Dunia inakauka na kunyauka; ulimwengu unafazaika na kunyauka; mbingu zinafazaika pamoja na dunia. Watu wameichafua dunia maana wamezivunja sheria za Mungu, wamegeuka mbali na masharti yake, wamelivunja agano lake la milele. Kwa sababu hiyo laana inaiteketeza dunia, wakaaji wake wanateseka kwa ajili ya makosa yao. Wakaaji wa dunia wamepunguka, ni watu wachache tu waliobaki. Mizabibu inanyauka, divai inakosekana. Wote waliokuwa wenye furaha sasa wanaugua kwa huzuni. Mudundo wa ngoma umekoma, makelele na fujo vimetoweka; midundo ya vinubi imekomeshwa. Hakuna tena kunywa divai na kuimba; kinywaji cha kulewesha kimekuwa uchungu kwa wakunywaji. Muji wa fujo umejaa uharibifu; kila nyumba imefungwa kusudi mutu asiingie. Kuna kilio katika barabara kwa kukosa divai; shangwe yote imekoma, furaha imetoweka katika dunia. Muji ni mabomoko matupu; milango yake imevunjwavunjwa. Kama vile zeituni chache tu juu ya mizeituni au tini chache tu juu ya muti wa tini, kisha kumaliza mavuno, ndivyo inavyokuwa katika inchi zote. Watu wanalalamika, wanaimba kwa shangwe. Kutoka upande wa magaribi, wanatangaza ukubwa wa Yawe, na wale wa upande wa mashariki wanamusifu. Watu wa mbali wanalisifu jina la Yawe, Mungu wa Israeli. Tunasikia nyimbo za sifa kutoka miisho ya dunia, nyimbo za kumusifu Mungu anayekuwa mwenye haki. Lakini mimi ninasema: Ninakonda, kweli ninakonda. Ole kwangu mimi! Wadanganyifu wanaendelea kuwa wadanganyifu, udanganyifu wao unazidi kuwa mubaya zaidi. Woga, mashimo na mitego, hivi ndivyo vinavyowangojea, enyi wakaaji wa dunia. Mutu atakayekimbia sauti ya woga atatumbukia ndani ya shimo; na mutu atakayetoka ndani ya shimo atanaswa katika mutego. Madirisha ya mbinguni yamefunguliwa, misingi ya dunia inatikisika. Dunia inavunjikavunjika, inapasuka na kutikiswatikiswa. Inapepesuka kama mulevi, inayumbayumba kama kibanda. Imelemewa na muzigo wa zambi zake nayo itaanguka wala haitasimama tena. Siku ile Yawe ataliazibu jeshi la anga vilevile na wafalme wa dunia. Wote watakusanywa kama wafungwa katika shimo; watafungwa katika kifungo pamoja kwa miaka mingi, na kisha muda huo atawaazibu. Kisha mwezi utafezeheka, nalo jua litapata haya ya kuangaza, maana Yawe wa majeshi atatawala kule Yerusalema katika mulima Sayuni; ataonyesha wazee wa watu wake utukufu wake. Wewe, ee Yawe, ndiwe Mungu wangu; nitakutukuza na kulisifu jina lako, kwa maana umetenda mambo ya ajabu; unaitimiza kwa uaminifu na kweli mipango uliyoipanga tangu zamani. Umeufanya muji kuwa lundo la mawe, muji wenye pango kuwa uharibifu. Nyumba za watu wageni zimetoweka, wala hazitajengwa tena upya. Kwa hiyo watu wenye nguvu watakutukuza, miji ya mataifa kali itakuogopa. Maana wewe umekuwa kimbilio kwa wazaifu, pango kwa wakosefu katika taabu zao. Wewe ni kimbilio wakati wa zoruba, kivuli wakati wa joto kali. Kweli pigo la watu wakali ni kali kama zoruba inayopiga ukuta; ni kama joto la jua juu ya inchi kavu. Lakini wewe unakomesha fujo ya wageni. Kama wingu linavyofifisha joto la jua, ndivyo unavyokomesha nyimbo za ushindi za watu wakali. Juu ya mulima Sayuni, Yawe wa majeshi atawafanyia watu wote karamu ya nyama zenye kunona na divai nzuri, nyama tamu zenye mafuta, pamoja na divai safi. Katika mulima huuhuu, Yawe ataliondoa wingu la huzuni lililowafunika watu wote, kifuniko cha uchungu juu ya mataifa yote. Bwana wetu Yawe atakiangamiza kifo milele! Atayafuta machozi katika nyuso za watu wote na kuondoa haya ya watu wake katika dunia yote. Yawe amesema hivyo. Siku ile, watu wote watasema: Huyu ndiye Mungu wetu! Tumemungojea atuokoe. Huyu ndiye Yawe tuliyemutazamia. Mukuje tufurahi na kushangilia kwa sababu ametuokoa. Yawe ataulinda mulima wa Sayuni, lakini watu wa Moabu watakanyagwakanyagwa ndani ya inchi yao kama nyasi katika shimo la mboleo. Watainyoosha mikono yao kama mutu anayejaribu kuogelea, lakini pamoja na bidii yao, Yawe ataporomosha kiburi chao. Atabomoa pango za miji ya Moabu yenye kuta ndefu na kuiangusha chini ndani ya mavumbi. Siku ile watu wataimba wimbo huu katika inchi ya Yuda: Sisi tuna muji imara: Mungu anatulinda kwa kuta na upango. Mufungue milango ya muji, taifa aminifu liingie; taifa linalotenda mambo ya haki. Ee Mungu, unawaweka katika amani wanaokuwa imara, unawaweka katika amani kwa sababu wanakutegemea. Mutumainie Yawe siku zote kwa maana yeye ni kikingio chetu kwa milele. Amewaporomosha waliokaa pande za juu, muji wenye utukufu ameuangusha mpaka chini, ameutupa mpaka katika mavumbi. Sasa muji huo unakanyagwakanyagwa kwa miguu ya watu wamasikini na wazaifu. Njia ya watu wa haki ni yenye kunyooka; ewe Mungu mwenye haki, unasawanisha njia yao. Katika njia ya maamuzi yako tunakungojea ee Yawe; tamaa yetu ni kulikumbuka jina lako. Moyo wangu unakutamani usiku kucha, nafsi yangu inakutafuta kwa moyo. Utakapohukumu dunia, watu wote katika ulimwengu watajifunza haki. Lakini waovu hata wakipewa rehema, hawawezi kujifunza kutenda haki. Hata katika inchi ya usawa, wao bado wanatenda maovu, wala hawajali ukubwa wako wewe Yawe. Ee Yawe umeinua mukono kwa kuwaazibu, lakini hawauoni. Uwaonyeshe namna unavyowapenda watu wako nao watapata haya. Moto unaowatayarishia waadui zako, uwateketeze! Wewe, ee Yawe, umetupatia amani; umefanikisha shuguli zetu zote. Ee Yawe, Mungu wetu, tulipata kutawaliwa na wabwana wengine ambao si wewe, lakini tunakubali wewe pekee kuwa Mungu wetu. Watu hao wamekufa, wala hawataishi tena; wamekuwa mizimu, wala hawatafufuka. Maana wewe umewaazibu na kuwaangamiza, hakuna atakayeweza kuwakumbuka tena. Umezidisha taifa letu, ee Yawe, umelizidisha taifa letu. Umeipanua mipaka yote ya inchi, kwa hiyo wewe unatukuzwa. Ee Yawe, walipotaabika walikutafuta, walikuomba musaada ulipowaazibu. Kama vile mama mwenye mimba anayezaa analia na kugaagaa kwa uchungu, ndivyo tulivyokuwa kwa sababu yako, ee Yawe. Sisi tulipata maumivu ya kuzaa, lakini tukazaa tu upepo! Hatukupata ushindi wowote kwa ajili ya inchi yetu, hatukuweza kuongeza hesabu ya watu katika inchi. Wafu wako wataishi tena, miili yao itafufuka. Wanaolala katika mavumbi wataamuka na kuimba kwa furaha! Mungu atapeleka umande wake wa uzima, nao wanaokuwa kwa wafu watatoka wazima. Mukuje watu wangu, muingie ndani ya nyumba zenu, mujifungie humo ndani. Mujifiche kwa muda mufupi, mpaka kasirani ya Yawe ipite. Maana Yawe anakuja kutoka kwake juu, kutoka makao yake huko mbinguni; kuwaazibu wakaaji wa dunia kwa uovu wao. Nayo dunia haitaficha tena wale waliouawa, lakini itaufichua umwagaji wa damu wote. Siku hiyo, Yawe atakamata upanga wake mukubwa, mukali na imara, na kuiazibu Leviatani, ile nyoka inayoruka na kuzongazonga. Yawe ataua nyoka mukubwa anayeishi katika bahari. Siku hiyo, muimbe juu ya shamba zuri la mizabibu: Mimi, Yawe, ni mulimaji wake; ninalimwangilia maji kila wakati. Ninalilinda usiku na muchana, kusudi lisiharibiwe na mutu yeyote. Silikasirikii tena shamba hili; kama miiba na michongoma ingelilishambulia, mimi ningepambana nayo na kuichoma kwa moto. Wakitaka ulinzi wangu, basi, wafanye amani nami. Wafanye amani nami! Itakuja siku wazao wa Yakobo watatoa mizizi; watu wa Israeli watachanua na kuchipuka, na kuijaza dunia yote kwa matunda. Mungu hakuwaazibu Waisraeli vikali kama alivyowaazibu waadui zao; Waisraeli waliouawa ni wachache kuliko wale waliokuwa wanawaua. Aliwaazibu watu wake kwa kuwapeleka katika uhamisho. Wakati wa upepo mukali wa mashariki, aliwaondoa kwa pigo kali. Hivi ndivyo uovu wa wazao wa Yakobo utakavyoondolewa, hivi ndivyo zambi yake itakavyofutwa kabisa: ataziharibu mazabahu za miungu; mawe yake yatasagwasagwa kama chokaa. Sanamu za Ashera wala mazabahu za kufukizia ubani hazitabaki. Muji ule wenye kuta sasa umekuwa mutupu, umeachwa na kuhamwa kama jangwa, humo ngombe wanakula na kupumzika. Matawi ya miti yamekauka na kuvunjika; wanawake wanayaokota na kuyawasha moto. Watu hawa hawajaelewa kitu, kwa hiyo Mungu, Muumba wao, hatawahurumia, yeye aliyewafanya, hatawatendea mema. Siku hiyo, Yawe atapepeta ngano yake kutokea kwenye muto Furati mpaka kwenye mupaka wa Misri, nanyi Waisraeli mutakusanywa mumojamumoja. Siku hiyo, baragumu kubwa itapigwa na watu wote wa Israeli waliopotea katika inchi ya Asuria au waliotawanywa katika inchi ya Misri watarudi na kumwabudu Yawe juu ya mulima mutakatifu kule Yerusalema. Ole wa Samaria, muji unaokuwa kama taji juu ya bonde kwenye udongo muzuri. Walevi wa ajabu wa Efuraimu wanajivuna kwa ajili yake, lakini utukufu wake utatoweka kama ua linalonyauka! Bwana amejichagulia mutu wake shujaa na mwenye nguvu, ambaye ni kama mvua ya mawe na zoruba kali, kama zoruba ya mafuriko makubwa; kwa mukono wake atawatupa chini. Majivuno na utukufu wa walevi wa Efuraimu vitakanyagwakanyagwa chini, utukufu wake unatoweka kama ua linalonyauka; utukufu uliotawala katika bonde kwenye udongo muzuri utakuwa kama tini za mwanzo mbele ya wakati wa mavuno; mutu akiziona anazichuma na kuzikula mara moja. Siku ile Yawe wa majeshi atakuwa taji tukufu, kama kitambaa kizuri kwa watu wake watakaobaki wazima. Atawaongoza waamuzi wa tribinali kuhukumu kwa haki, nao walinzi wa muji atawapa nguvu. Lakini kuna wengine waliolewa divai na kuyumbayumba kwa sababu ya pombe kali; makuhani na manabii wamelewa pombe kali, wamevurugika kwa divai. Wanayumbayumba kwa pombe kali; maono yao yamepotoka, wanajikwaa katika kutoa hukumu. Meza zote zimejaa matapiko, hakuna pahali popote palipo safi. Wao wananichekelea na kuuliza: Huyu nabii anataka kufundisha nani? Anazani atatuelezea sisi ujumbe wake? Sisi ni watoto wachanga walioachishwa kunyonya juzijuzi? Anatufundisha kama watoto wadogo: kanuni juu ya kanuni, mustari juu ya mustari; mara hiki, mara hiki! Basi! Yawe ataongea na watu hawa kwa njia ya watu wa luga tofauti wanaoongea luga ngeni. Yeye alikuwa amewaahidia ninyi: Nitawaonyesha ninyi pumziko, nitawapa pumziko enyi muliochoka. Hapa ni pahali pa pumziko. Lakini wao hawakutaka kunisikiliza. Basi Yawe atawafundisha kama watoto wadogo: kanuni juu ya kanuni, mustari juu ya mustari; mara hiki, mara hiki! Nao watalazimishwa kukimbia lakini wataanguka machalichali, watavunjika, watanaswa na kutekwa. Basi, musikilize neno la Yawe, enyi wenye mazarau munaotawala watu wa Yerusalema: Ninyi munajidai mumefanya agano na kifo mumefanya mapatano na kuzimu! Ninyi munasema kwamba hasara itakapokuja haitawapata, kwa sababu mumefanya uongo kuwa tegemeo lenu, na udanganyifu kuwa kikingio chenu! Basi, Bwana wetu Yawe anasema hivi: Ninaweka katika Sayuni jiwe la musingi, jiwe ambalo limeimarishwa. Jiwe la pembe, la bei kali, jiwe ambalo ni la musingi imara; jiwe linalokuwa na maandiko haya: Anayeamini hataanguka. Nitatumia sheria kama kipimo changu, nitatumia haki kama timazi. Mvua ya mawe itaufagilia mbali uongo munaoutegemea, na mafuriko yataharibu kikingio chenu. Halafu agano lenu na kifo litavunjika, na mapatano yenu na kuzimu yatafutwa. Ile hasara kubwa itakapokuja itawaangusha chini. Kila mara itakapopita kwenu itawapata; nayo itapita kila asubui, muchana na usiku. Kusikia ujumbe huu tu kutakuwa kitisho. Kwenu itakuwa kama anayejinyoosha juu ya kitanda kifupi sana, au kujifunika kwa blanketi inayokuwa ndogo sana! Maana Yawe atasimama kama kule kwenye mulima Perasimu; atawaka hasira kama kule katika bonde la Gebeoni. Atatimiza mupango wake wa ajabu; atatenda kazi yake ya ajabu sana. Basi, ninyi musikuwe na mazarau vifungo vyenu visipate kukazwa zaidi. Maana nimesikia kwamba Yawe wa majeshi amekusudia kuiangamiza inchi yote. Mutege sikio, musikilize maneno ninayowaambia; musikilize vema hotuba yangu. Mulimaji anayetaka kupanda mbegu anaendelea kulima tu siku zote? Anaendelea kutipua na kusawanisha shamba lake? Hapana! Akisha kusawanisha shamba lake, anapanda mbegu za kunde na mbegu za vikolezo, anapanda ngano na shayiri kwa mustari, na kwenye mipaka ya shamba mimea mingine. Mutu huyo anajua kufanya vile, kwa sababu Mungu wake anamufundisha. Kunde haipepetwi kwa chombo kikali wala mbegu za vikolezo kwa gari! Lakini kunde zinapepetwa kwa fimbo na mbegu za vikolezo kwa kijiti. Mulimaji anapopepeta ngano yake, haendelei kuipepeta mpaka kuvunja punje zake. Anajua jinsi ya kuipepeta kwa gurudumu la gari, bila kuharibu punje za ngano. Ujuzi huu nao unatoka kwa Yawe wa majeshi. Mipango yake ni ya ajabu, hekima yake ni kamilifu kabisa. Ole kwako Yerusalema, mazabahu ya Mungu, muji ambamo Daudi alipiga kambi yake! Miaka inakuja na kupita, na sikukuu zako zinaendelea kufanyika; lakini mimi Mungu nitahuzunisha Yerusalema, ndani yake kutakuwa vilio na maombolezo, muji wenyewe utakuwa kama mazabahu. Mimi nitapanga kundi la waaskari juu ya Yerusalema, nami nitauzunguka na kuushambulia. Utaangushwa mbali sana ndani ya udongo, kutoka kule mbali utatoa sauti, maneno yako yatatoka kule chini katika mavumbi, sauti yako itatoka ndani ya udongo kama ya muzimu. Kundi la waadui zako litakuwa kama mavumbi laini, waliokutendea ukali watakuwa kama maganda. Hayo yatafanyika kwa rafla. Yawe wa majeshi atakuja kukusaidia; atakuja na ngurumo, tetemeko la inchi na sauti kubwa; atakuja na upepo mukali, zoruba na moto wenye kuunguza. Halafu, kundi la mataifa yote yanayoshambulia Yerusalema, wote wanaoshambulia ukuta wake na kuutia wasiwasi, watatoweka kama ndoto, kama maono ya usiku. Mataifa yote yanayoshambulia Yerusalema yatakuwa kama mutu mwenye njaa anayeota ndoto kwamba anakula lakini anaamuka angali bado na njaa, na kama mutu mwenye kiu anayeota kwamba anakunywa lakini anaamuka muzaifu, na angali bado na kiu. Mukuwe wapumbafu na kupumbazika: mupofuke na kuwa vipofu! Mulewe lakini si kwa divai; mupepesuke lakini si kwa pombe. Yawe amewamwangia roho ya usingizi; macho yenu yasipate kuona enyi manabii, amefunika vichwa vyenu enyi wenye kupata maono. Basi, kwenu ninyi, maono haya yote ni kama ujumbe ulioandikwa katika kitabu kilichofungwa kwa muhuri. Ukimupelekea mutu yeyote anayejua kusoma, na kumwambia “Unisomee kitabu hiki”, atasema “Siwezi kukisoma kwa sababu kimefungwa kwa muhuri.” Na ukimupa mutu yeyote asiyejua kusoma, na kumwambia “Unisomee kitabu hiki”, atasema: “Sijui kusoma.” Bwana anasema: Watu hawa wanakuja kuniabudu kwa maneno tu, lakini mioyo yao iko mbali nami. Wananiheshimu kulingana na desturi ya watu tu, jambo walilojifunza wao wenyewe. Hivyo, nitawatendea tena watu hawa maajabu, mambo ya ajabu na ya kushangaza. Nao wenye hekima wao wataishiwa hekima, na akili ya wenye akili wao itatoweka. Ole kwenu ninyi munaomuficha Yawe mipango yenu, munaotenda matendo yenu katika giza na kusema: Hakuna atakayetuona; nani anayeweza kujua tunachofanya? Ninyi munafanya mambo kinyume kabisa! Mufinyanzi na udongo ni hali moja? Chombo hakiwezi kumwambia aliyekitengeneza hivi: Wewe haukunitengeneza. Kilichofinyangwa hakiwezi kumwambia aliyekiumba; Wewe haujui kitu. Bado kidogo tu, pori la Lebanoni litageuzwa kuwa shamba lenye udongo muzuri, na shamba lenye udongo muzuri kuwa pori. Siku hiyo viziwi watasikia ujumbe ukisomwa katika kitabu na kutoka katika giza, vipofu wataanza kuona. Wanyenyekevu watapata furaha mupya kwa Yawe, na wamasikini kati ya watu watashangilia kwa furaha, kwa sababu ya Mungu, Mutakatifu wa Israeli. Watesaji watatoweka, wenye kumuchekelea Mungu watakwisha, wote wanaokusudia kutenda maovu watateketezwa. Watatoweka wale wanaopotosha maneno ya mutu katika tribinali, watu wanaowatega waamuzi na wanaosema uongo kwa kuwanyima haki yao wasiokuwa na kosa. Kwa hiyo, Yawe aliyemukomboa Abrahamu, anasema hivi juu ya wazao wa Yakobo: Wazao wa Yakobo hawatapata haya tena, hawatainamisha vichwa vyao tena kwa ajili ya haya. Watakapowaona watoto wao, watoto niliowajalia mimi mwenyewe, watalitukuza jina langu mimi Mutakatifu wa Yakobo, watakuwa na heshima kwangu mimi Mungu wa Israeli. Waliopotoka katika roho watapata maarifa na wenye kunungunika watakubali kufundishwa. Ole watoto waasi, wanaotimiza mipango yao na si mipango yangu, wanaofanya mapatano kinyume cha mapenzi yangu! –Ni ujumbe wa Yawe.– Kweli, wanalundika zambi juu ya zambi. Bila kutaka shauri langu, wanafunga safari kwenda Misri, kukimbilia ulinzi kwa mufalme wa Misri, kupata pahali pa kujificha katika inchi yake. Lakini ulinzi wa Mufalme wa Misri utakuwa haya yenu, na kujificha katika inchi ya Misri kutakuwa fezeha yenu. Maana ingawa wakubwa wao wamefika Soani, na wajumbe wao mpaka katika muji wa Hamesi, wote watapata haya. Wamisri hawawezi kuwasaidia ninyi, hawawezi kuwapa musaada au faida, lakini watawapatisha haya tu na kuwafezehesha. Ujumbe wa Mungu juu ya nyama wa pande za jangwa ya kusini: Wajumbe wanapita katika inchi ya taabu na shida, yenye simba, nyoka wa sumu na nyoka wakubwa wanaoruka. Wamewabebesha punda na ngamia wao mali zao, kuwapelekea watu wasioweza kuwafalia kitu. Maana musaada wa Misri ni bure, haufai kitu; kwa hiyo nimeipanga Misri jina: Nyoka mukubwa asiyekuwa na nguvu! Mungu aliniambia: Sasa andika jambo hili mbele yao, juu ya kibao na katika kitabu, likuwe ushuhuda wa milele: Watu hawa ni waasi, watoto wasioaminiwa; watu wasiopenda kusikia mafundisho ya Yawe. Wanawaambia wale wanaopata maono hivi: Musipate maono. Wanawaambia manabii hivi: Musitutangazie ukweli, lakini mutuambie mambo ya kupendeza, mutoe unabii wa mambo ya udanganyifu tu. Mugeuke na kuiacha njia ya ukweli; musituambie tena juu ya Mungu, Mutakatifu wa Israeli. Kwa hiyo Mungu, Mutakatifu wa Israeli, anasema hivi: Ninyi mumeukataa ujumbe wangu; mukatumainia kutenda mabaya na kutengeneza udanganyifu. Basi, zambi hii itakuwa kwenu kama ufa mukubwa katika ukuta murefu; utabomoka mara moja na kuanguka chini kwa rafla. Kuporomoka kwa ukuta huo, ni kama kupasuka kwa chungu ambacho kimepasuliwa vibaya sana, bila kubaki kigae cha kuopolea moto ndani ya jiko, au kuchotea maji katika kisima. Bwana wetu Yawe, Mutakatifu wa Israeli anasema hivi: Mukinirudilia na kutulia mutaokolewa; kwa utulivu na kunitumainia mutapata nguvu. Lakini ninyi hamukutaka. Pahali pake mulisema: Hapana! Sisi tutakimbia na farasi wenye mbio. Sawa, mutakimbia na farasi wenye mbio, lakini farasi wa waadui zenu wana mbio zaidi. Watu wenu elfu moja watamukimbia askari mumoja adui; na waaskari watano waadui watawakimbiza ninyi wote. Kwa mwisho, watakaobaki, watakuwa kama muti wa bendera kwa mulima, kama kitambulisho kinachokuwa juu ya kilima. Hata hivyo, Yawe anangoja kuwasamehe, atasimama na kuwaonea huruma. Yawe ni Mungu wa haki. Heri wote wale wanaomutumainia. Enyi watu wa Sayuni, enyi watu wa Yerusalema, hakika ninyi hamutaomboleza tena. Kweli Mungu atawahurumia; mara tu atakaposikia kilio chenu atawaitikia. Ingawa Bwana atawakulisha chakula cha taabu na kuwakunywesha maji ya mateso, yeye ndiye Mwalimu wenu na hatajificha tena; nanyi mutamwona kwa macho yenu wenyewe. Mukienda kwa upande wa kuume au kushoto, mutasikia sauti nyuma yenu ikisema: Njia ni hii; muifuate. Mutazihesabu sanamu zenu za miungu zilizopakwa feza na zahabu kuwa uchafu. Mutazitupilia mbali kama takataka, mukisema: Mupotelee mbali! Mutakapopanda mbegu zenu, Yawe atanyesha mvua kwa wakati wake, nazo zitakomaa na kuwapa mavuno mengi mazuri. Makundi yenu ya nyama nao watakula katika mashamba makubwa ya kukulishia nyama. Ngombe dume na punda wenu wa kulima watapata malisho yaliyochaguliwa vizuri na kutiwa chumvi. Wakati utakapofika ambapo waadui watauawa na minara yao kubomolewa, vijito vya maji vitatiririka kutoka kila mulima na kilima. Tena mwezi utawaka kama jua, nao mwangaza wa jua utakuwa mara saba ya mwangaza wake wa kawaida, sawa vile kwamba mwangaza wa siku saba umeangaza katika siku moja. Mambo haya yote yatatukia wakati Yawe atakapofunga vidonda na kuponyesha mapigo aliyowaletea watu wake. Muangalie, Yawe mwenyewe anakuja tokea mbali! Amewaka hasira na moshi unafuka; midomo yake inaonyesha kasirani yake, maneno anayosema ni kama moto unaoteketeza. Pumzi yake ni kama mafuriko ya muto ambao maji yake yanafika mpaka kwenye shingo. Anakuja kupepeta mataifa kwa lungo ya maangamizi, kuwafunga lijamu na kuwapeleka wasikotaka. Lakini ninyi watu wa Yerusalema mutaimba kwa furaha kama munavyofanya wakati wa makesha ya sikukuu. Mutajaa furaha kama watu wanaotembea kwa mudundo wa muziki wa filimbi kwenda kwenye mulima kwa Yawe, kikingio cha Israeli. Yawe atawafanya watu wote waisikie sauti yake tukufu na pigo la nguvu yake lionekane kwa hasira nyingi. Kutakuwa ndimi za moto mukali, ngurumo, zoruba na mvua ya mawe. Waasuria watajaa hofu watakaposikia sauti ya Yawe, wakati atakapowapiga na fimbo yake. Kila pigo la azabu ya Yawe juu ya Waasuria litaandamana na mudundo wa ngoma na zeze. Yeye mwenyewe atapigana na Waasuria. Kweli, pahali pa kumuteketeza mufalme wa Asuria pamekwisha kutayarishwa muda murefu uliopita. Pahali penyewe ni shimo kubwa na pana. Kuna moto na kuni kwa uwingi. Yawe ataupulizia pumzi yake kama kijito cha kiberiti na kuuwasha. Ole kwao wale wanaokwenda Misri kuomba musaada! Wanategemea farasi, wanategemea wingi wa magari ya vita na nguvu za waaskari wao wapanda-farasi. Lakini hawamutegemei Mutakatifu wa Israeli, wala hawamwombi Yawe shauri! Mungu ni mwenye hekima na analeta maangamizi. Habadilishi masemi yake; lakini yuko tayari kuwaazibu watu waovu vilevile na wasaidizi wa watenda mabaya. Wamisri ni wanadamu tu wala si miungu; farasi wao nao ni nyama tu, si roho. Yawe akiunyoosha mukono wake, taifa linalotoa musaada litajikwaa, na lile linalosaidiwa litaanguka; yote mawili yataangamia pamoja. Yawe aliniambia hivi: Simba mukali ananguruma kwa kukinga nyama aliyemukamata; hata kundi la wachungaji likiitwa kwa kumufukuza, hatishiki kwa kelele zao, wala hashituki kwa sauti zao. Ni vile Yawe wa majeshi atakavyoshuka kupigana juu ya mulima Sayuni na kilima chake. Kama vile ndege anavyonyoosha mabawa juu ya vitoto vyake, ni vile Yawe atakavyolinda Yerusalema. Ataulinda na kuukomboa, ataukinga na kuuokoa. Enyi Waisraeli, mumurudilie yule muliyemwacha kabisa. Wakati utafika ambapo ninyi wote mutatupilia mbali sanamu zenu za feza na zahabu ambazo mumejitengenezea kwa mikono yenu inayowakosesha. Hapo Waasuria watauawa kwa upanga, lakini si upanga wa watu; wataangamizwa kwa upanga ambao ni zaidi ya ule wa wanadamu. Waasuria watakimbia na vijana wao watatumikishwa kazi za kitumwa. Mufalme wao atatoroka kwa ajili ya hofu, na wakubwa wao wataiacha bendera yao kwa ajili ya woga. –Ni ujumbe wa Yawe ambaye moto wake uko katika Sayuni, ambaye furu lake liko katika Yerusalema. Kutatokea mufalme atakayetawala kwa haki, nao wakubwa wataongoza kwa kufuatana na sheria ya Mungu. Kila mumoja atakuwa kama pahali pa kujikinga na upepo, kama pahali pa kujificha wakati wa mvua kubwa. Watakuwa kama vijito vya maji katika inchi yenye kukauka, kama kivuli cha jiwe kubwa katika jangwa. Macho ya wanaoona hayatapofushwa tena, masikio ya wanaosikia yatabaki wazi. Mioyo ya wasiofikiri itapata ufahamu, wenye vigugumizi watasema upesi. Wapumbafu hawataitwa tena wenye cheo, wala watu wa ovyoovyo hawataitwa tena waheshimiwa. Wapumbafu wanasema maneno ya upumbafu, na mafikiri yao ni kutenda maovu, kutenda mambo ya watu wasiomujua Mungu, kusema maneno ya kumutukana Yawe. Wanawaacha wenye njaa bila chakula, na wenye kiu wanawanyima kinywaji. Matendo ya watu wadanganyifu ni mabaya; hao wanatunga maneno mabaya kwa kumwangamiza masikini kwa maneno ya uongo, hata kama masikini ni mwenye sheria. Lakini wenye heshima wanatenda mambo ya heshima, nao wanatetea mambo yenye heshima. Musimame, enyi wanawake munaostarehe, munisikilize; musikilize maneno ninayosema, enyi wabinti musiojali kitu. Katika mwaka mumoja hivi mutatetemeka ninyi muliotosheka; maana hamutapata mavuno yoyote, na mavuno ya mizabibu yatatoweka. Mutetemeke kwa woga, enyi munaojiikalia tu; mutetemeke kwa hofu, enyi munaostarehe! Muvue nguo zenu, mubakie uchi, mujifungie nguo ya gunia katika viuno vyenu. Mujipige kifua kwa huzuni, muomboleze, juu ya mashamba yaliyokuwa mazuri, juu ya mizabibu iliyokuwa ikizaa sana, juu ya inchi ya watu wangu inayoota miiba na michongoma, juu ya nyumba zote zilizojaa watu wenye furaha, juu ya muji uliokuwa na shangwe. Maana nyumba ya kifalme itaachwa ukiwa, muji huo wa watu wengi utahamwa. Mulima na munara wa ulinzi utakuwa mapango milele, punda wa mwitu watapitapita huko kwa furaha, kondoo watapata malisho yao humo. Hali itaendelea kuwa hivyo mpaka tujazwe Roho wa Mungu kutoka juu. Hapo jangwa litakuwa shamba lenye udongo muzuri tena, na mashamba yenye udongo muzuri yatakuwa pori. Katika inchi jangwa, watu watafuata sheria ya Mungu, katika mashamba yenye udongo muzuri, watatenda kwa haki. Kutokana na kutenda kwa haki, watu watapata amani, utulivu na usalama kwa milele. Watu wangu watakaa katika makao ya amani, katika pahali penye usalama na nafasi yenye utulivu. Lakini mvua ya mawe itanyesha na kuangusha pori, na muji wake utaangamizwa. Lakini heri yenu ninyi: mutapanda mbegu zenu popote penye maji, ngombe na punda wenu watatembeatembea namna wanavyotaka. Ole kwako! Unaangamiza ingawa hauangamizwi. Unadanganya ingawa haudanganywi. Utakapokwisha kuangamiza, wewe utaangamizwa! Utakapomaliza kudanganya, wewe utadanganywa. Ee Yawe, utuonee huruma, kwako tumeliweka tumaini letu. Ukuwe kikingio chetu kila siku, mwokozi wetu wakati wa taabu. Kwa kishindo cha sauti yako watu wanakimbia; unaposimama tu, mataifa yanatawanyika. Waadui zao wanakusanya vitu walivyonyanganya, wanavirukia kama mapanzi. Yawe ametukuzwa, yeye anaishi juu mbinguni. Ameujaza Sayuni usawa na haki. Enyi watu wa Yerusalema, Yawe atawajalia usalama, atawaokoa na kuwapa hekima na maarifa. Akiba yenu kubwa ni kumwogopa Yawe. Muangalie, washujaa wao wanalia, wajumbe wa amani wanaomboleza. Barabara kubwa zimebaki tupu; hakuna anayesafiri kupitia ndani yao. Mapatano yanavunjwa ovyo, washuhuda wanazarauliwa. Hakuna anayejali tena maisha ya wanadamu. Inchi inaomboleza na kunyauka; pori ya Lebanoni imekauka, bonde zuri la Saroni limekuwa jangwa, kule Basani na mulima Karmeli majani yote yamekauka. Yawe anasema hivi: Sasa mimi nitasimama; sasa nitajiweka tayari; sasa mimi nitatukuzwa. Mipango yenu yote ni kama maganda, na matokeo yake ni takataka tupu. Pumzi yangu itawaangamiza kama moto. Watu watakuwa kama wamechomwa kuwa majivu, kama miiba iliyokatwa na kuteketezwa katika moto. Musikilize mambo muliyofanya, enyi munaokuwa mbali; nanyi munaokuwa karibu, mutambue uwezo wangu. Wenye zambi katika Sayuni wanaogopa, wasiomwamini Mungu wanatetemeka na kusema: Nani anayeweza kuvumilia moto huu mukali? Nani anayeweza kuvumilia ndimi za moto usiozimika? Ni mutu anayekuwa hivi: anaishi kwa haki na kusema kwa usawa, anazarau kabisa utajiri wa unyanganyi, anakataa kupokea kituliro, hakubali hata kidogo kusikia mipango ya mauaji, wala hakubali macho yake yaone maovu. Mutu wa namna hiyo anaishi kwenye nafasi ya juu, pahali salama, penye pango na mawe makubwa; atapewa chakula chake siku zote, na maji yake ya kunywa hayatakosekana. Mutaweza kumwona mufalme katika utukufu wake, mutaiona inchi anayotawala, kubwa na pana. Mutakumbuka kitisho kilichopita na kujiuliza: Wako wapi wale waliokadirisha na kuchunguza kodi? Wako wapi wale waliopeleleza ugumu wa kuta zetu? Hamutawaona tena watu wale wenye kiburi, wanaozungumuza luga isiyoeleweka. Muangalie Sayuni tunamofanyia sikukuu zetu; muangalie Yerusalema, makao matulivu, hema imara; misumari yake haitaongolewa hata kidogo, kamba zake hazitakatwa hata moja. Humo Yawe atatuonyesha ukubwa wake. Kutakuwa mito mikubwa na vijito, lakini mashua za vita hazitapita, wala mashua kubwa kuingia. Maana Yawe ni mwamuzi wetu, yeye ni mutawala wetu; Yawe ni mufalme wetu, yeye ndiye anayetuokoa. Ewe Sayuni, kamba zako zimeregea, haziwezi kushikilia matanga yake, wala kufungia paa zao. Lakini vitu vingi vilivyonyanganywa vitagawanywa; hata vilema wataweza kupata sehemu yao. Hakuna atakayesema tena ni mugonjwa; watu watasamehewa uovu wao wote. Mujongee musikilize enyi mataifa, musikilize enyi watu. Sikiliza, ee dunia na vyote vinavyokuwa ndani yake, ulimwengu na vyote vinavyotoka humo! Yawe amekasirikia mataifa yote, amekasirikia majeshi yao yote. Ameyapangia mwisho wao, ameyatoa yaangamizwe. Maiti zao zitatupwa inje; harufu ya maiti zao itasambaa; damu yao itatiririka juu ya milima. Jeshi lote la anga litaharibika, anga zitakunjamana kama karatasi. Jeshi lake lote litanyauka, kama vile majani ya mizabibu au mitini yanavyonyauka. Upanga wa Mungu uko tayari juu mbinguni. Angalia, unashuka kuwaazibu Waedomu, watu ambao ameamua kuwaangamiza. Upanga utajaa damu na mafuta: damu ya kondoo na mbuzi, na mafuta ya figo za kondoo dume. Maana Yawe ana sadaka huko Bosira, kutakuwa mauaji makubwa katika inchi ya Edomu. Mbogo wataangamizwa pamoja nao, wana-ngombe pamoja na ngombe dume. Inchi italewa na damu, udongo utashiba kwa mafuta yao. Maana Yawe yuko na siku ya kulipiza kisasi; mwaka wa kulipiza waadui za Sayuni. Vijito vya Edomu vitatiririsha kabulimbo, udongo wake utakuwa kiberiti; inchi yake itakuwa kabulimbo inayowaka. Itawaka usiku na muchana bila kuzimika, moshi wake utapanda juu milele. Inchi itakuwa jangwa siku zote, hakuna atakayepitia huko milele. Itakuwa makao ya ndege za jangwa: kozi, bundi na kibombobombo. Yawe atawaletea muvurugano, na timazi la fujo kwa wakubwa wake. Inchi itaitwa Inchi bila Mufalme; wakubwa wake wote wametoweka. Miiba itaota katika pango zake, miiba na michongoma ndani ya kuta zake. Itakuwa makao ya imbwa wa pori, nafasi ya mbuni. Paka wa pori na fisi watakuwa humo, mapepo wataitana humo; sulukutu atatulia humo na kupata nafasi ya kupumzika. Humo bundi watataga mayai na kuyaatamia, watatotoa vitoto na kuviweka chini ya kivuli chao. Humo tai watakutanana, kila mumoja na mwenzake. Musome katika kitabu cha Yawe: Hakuna hata kiumbe kimoja kitakachokosekana, kila kimoja kitakuwa na mwenzake. Maana kinywa cha Yawe kimeamuru hivyo. Roho yake itawakusanya hao wote. Yawe amepanga sehemu ya kila mumoja wao, ametumia kamba kuwapimia inchi hiyo; watairizi milele na milele, wataishi mule kizazi hata kizazi. Mbuga na inchi kavu vitachangamuka, jangwa litafurahi na kuchanua maua. Litachanua maua kwa wingi kama waridi, litashangilia na kuimba kwa furaha. Mungu atalijalia utukufu wa milima ya Lebanoni, uzuri wa mulima Karmeli na wa bonde la Saroni. Watu watauona utukufu wa Yawe, watauona ukubwa wa Mungu wetu. Muimarishe mikono zaifu, mukaze magoti yanayoregea. Muwaambie waliovunjika moyo: Mujipe moyo, musiogope! Muangalie Mungu wenu atakuja kulipiza kisasi, atakuja kuwaazibu waadui zenu; atakuja yeye mwenyewe kuwaokoa ninyi. Hapo vipofu wataona tena, na viziwi watasikia tena. Viwete watarukaruka kama paa, na bubu wataimba kwa furaha. Maji yatabubujika katika jangwa na vijito katika mbuga. Muchanga wa moto katika jangwa utakuwa ziwa la maji, inchi kavu itabubujika vijito. Makao ya imbwa wa pori yatajaa maji; nyasi zitaota na kukomaa kama mianzi. Humo kutakuwa barabara kubwa, nayo itaitwa Njia Takatifu. Watu wachafu hawatapitia humo, lakini wale watu wa Mungu tu; wapumbafu hawatakanyaga ndani yake, humo hamutakuwa simba, nyama yeyote mukali hatapitia humo, hao hawatapatikana humo. Lakini waliokombolewa ndio watakaopita humo. Waliokombolewa na Yawe watarudi, watakuja Sayuni wakipiga vigelegele. Watakuwa wenye furaha ya milele, watajaliwa furaha na shangwe; huzuni na kilio vitatoweka kabisa. Katika mwaka wa kumi na ine wa utawala wa mufalme Hezekia, mufalme Saniharibu wa Asuria aliishambulia miji yote yenye kuta ya inchi ya Yuda na kuinyanganya. Kisha mufalme wa Asuria alimutuma jemadari kutoka Lakisi na kundi kubwa kumwendea mufalme Hezekia. Jemadari yule alisimama karibu na mufereji wa birika linalokuwa upande wa juu katika barabara kubwa inayoelekea shamba la wafuaji wa nguo. Nao walikutana na Eliakimu mwana wa Hilkia, aliyekuwa musimamizi wa nyumba ya kifalme, Sebuna, aliyekuwa katibu, pamoja na mwandishi Yoa mwana wa Asafu. Halafu yule jemadari wa Asuria aliwaambia: “Mumwambie Hezekia kwamba mufalme mukubwa wa Asuria anamwuliza: Unategemea nini kwa kukazana kwako? Unazani kwamba maneno matupu ndiyo maarifa na nguvu katika vita? Ni nani unayemutegemea hata ukaniasi? Angalia sasa. Unategemea Misri, utete uliovunjika ambao utamuchoma mukono yeyote atakayeuegemea. Hivi ndivyo mufalme wa Misri anavyokuwa kwa wote wale wanaomutegemea. Lakini hata kama mukiniambia ‘Tunamutegemea Yawe, Mungu wetu’, si huyohuyo ambaye Hezekia aliziharibu nafasi zake zote za kuabudu kwenye vilima pamoja na mazabahu zake na kuwaambia watu wa Yuda na Yerusalema: Munapaswa kuabudu mbele ya mazabahu hii ya Yerusalema tu? Basi, mufanye mapatano na bwana wangu mufalme wa Asuria. Mimi nitawapatia farasi elfu mbili, kama mutaweza kupata waaskari wapanda-farasi. Hata kama munategemea Misri kupata magari ya vita na waaskari wapanda-farasi, hamuwezi kumurudisha nyuma mutu mumoja wa cheo cha chini sana kati ya watumishi wa bwana wangu. Zaidi ya hayo, munafikiri nimekuja bila amri ya Yawe kwa kuishambulia na kuiangamiza inchi hii? Yawe ndiye aliyeniambia: ‘Ushambulie inchi hii na kuiangamiza!’ ” Kisha Eliakimu, Sebuna na Yoa wakamujibu yule jemadari: “Tafazali useme nasi kwa luga ya Kiaramea maana tunaielewa. Usiseme nasi kwa luga ya Kiebrania. Watu wanaokuwa juu ya ukuta wanasikia.” Yule jemadari akawaambia: “Munazani kwamba bwana wangu amenituma kutoa ujumbe huu kwa bwana wenu na kwenu tu? Maneno yangu ni vilevile kwa watu wanaoikaa juu ya ukuta! Bado kidogo wao kama vile ninyi watakula mavi yao wenyewe na kunywa mikojo yao wenyewe!” Kisha huyo jemadari akasimama, akalalamika na kusema kwa luga ya Kiebrania: “Musikilize maneno ya mufalme mukubwa, mufalme wa Asuria! Hivi ndivyo mufalme anavyosema: Musikubali Hezekia awadanganye, kwa sababu hataweza kuwaokoa. Musikubali awashawishi kusudi mumutegemee Yawe, akisema: ‘Yawe atatuokoa na muji huu hautatiwa katika mikono wa mufalme wa Asuria.’ Musimusikilize Hezekia, maana mufalme wa Asuria anasema: Mukuwe na amani nami na kujitoa kwangu. Kisha kila mumoja wenu ataweza kula matunda ya mizabibu yake mwenyewe na matunda ya tini yake mwenyewe na kunywa maji ya kisima chake mwenyewe, mpaka nitakapokuja na kuwapeleka katika inchi kama hii yenu, inchi yenye ngano na divai, inchi yenye mukate na mashamba ya mizabibu. Musimusikilize Hezekia anapowadanganya akisema: ‘Yawe atatuokoa.’ Kuna yoyote kati ya miungu ya mataifa aliyeokoa inchi yake toka katika mikono ya mufalme wa Asuria? Iko wapi ile miungu ya Hamati na Arpadi? Iko wapi ile miungu ya Sefarwaimu? Imeokoa Samaria toka katika mikono yangu? Ni nani kati ya miungu ya inchi hizi aliyeokoa inchi zao toka katika mikono yangu. Yawe ataweza kuuokoa Yerusalema?” Lakini watu walinyamaza, wala hawakumujibu neno kama vile walivyoamuriwa na mufalme akisema: “Musimujibu.” Kisha Eliakimu mwana wa Hilkia aliyekuwa musimamizi wa nyumba ya kifalme, Sebuna aliyekuwa katibu, na Yoa mwana wa Asafu mwandishi, wakamwendea Hezekia na nguo zenye kupasuliwa, wakamwelezea maneno ya yule jemadari. Mufalme Hezekia aliposikia habari hiyo, alipasua nguo yake, akavaa nguo ya gunia, akaingia katika nyumba ya Yawe. Aliwaamuru Eliakimu, musimamizi wa nyumba ya kifalme, Sebuna, katibu, na wazee wa makuhani, wamwendee nabii Isaya mwana wa Amozi, wakiwa wamevaa nguo za magunia. Nao wakamwambia Isaya: “Hezekia anasema hivi: Leo ni siku ya huzuni, ya kuazibiwa, na ya kuzarauliwa. Sisi tumekuwa kama mwanamuke anayetaka kuzaa mutoto, lakini hana nguvu ya kumuzaa. Labda Yawe, Mungu wako, alisikia maneno ya yule jemadari ambaye ametumwa na bwana wake mufalme wa Asuria, kwa kumutukana Mungu Mwenye Uzima, naye Yawe, Mungu wako atamwazibu kwa ajili ya maneno aliyoyasikia. Uwaombee watu wanaobaki.” Basi, hao watumishi wa mufalme Hezekia walipokwisha kufika kwa Isaya, aliwaambia: “Mumwambie bwana wenu kwamba Yawe anasema hivi: Usiogope kwa sababu ya maneno uliyoyasikia, ambayo watumishi wa mufalme wa Asuria wameyasema kwa kunitusi. Sikia, nitamufanya mufalme asikie uvumi, halafu atarudi katika inchi yake, na kule nitamufanya auawe kwa upanga.” Kisha yule jemadari aliposikia kwamba mufalme wa Asuria alikuwa ameondoka Lakisi, aliondoka na kumukuta akishambulia muji wa Libuna. Halafu mufalme alipata habari kwamba Tiraka mufalme wa Etiopia anakuja kupigana naye. Akatuma wajumbe kwa Hezekia, akisema: “Mumwambie Hezekia mufalme wa Yuda: Usikubali Mungu wako unayemutegemea akudanganye kwa kukuahidi kwamba Yerusalema hautatekwa na mufalme wa Asuria. Wewe umekwisha kusikia jinsi wafalme wa Asuria walivyotendea inchi nyingine na kuziangamiza kabisa. Unazani wewe utaokoka? Miungu ya mataifa iliokoa Gozani, Harani, Resefu na Waedeni waliokaa Terasari, mataifa ambayo babu zangu waliyaangamiza? Wako wapi wafalme wa Hamati, Arpadi, Sefarwaimu, Hena na Iva?” Mufalme Hezekia alipokea barua kutoka kwa wajumbe na kuisoma. Kisha akaenda na kuingia katika nyumba ya Yawe, akaiweka mbele ya Yawe. Halafu akamwomba Yawe akisema: “Ee Yawe wa majeshi, Mungu wa Israeli, unayeikaa katika kiti cha kifalme juu ya makerubi, ni wewe tu unayekuwa Mungu, unayetawala falme zote za ulimwengu. Wewe uliumba dunia na mbingu. Ee, Yawe, fungua macho uone, tega sikio lako uyasikie matusi yote ambayo Saniharibu amepeleka na kukutukana wewe Mungu Mwenye Uzima. Ee Yawe, ni kweli kwamba wafalme wa Asuria wameangamiza mataifa yote na inchi zao. Walitupa miungu yao katika moto kwa sababu haikukuwa miungu ya kweli, lakini sanamu za miti na mawe zilizochongwa na mikono ya watu. Sasa, ee Yawe, Mungu wetu, utuokoe toka katika makucha ya Saniharibu, kusudi falme zote za dunia zijue kwamba ni wewe peke yako, ee Yawe, ambaye ni Mungu.” Kisha Isaya mwana wa Amozi alituma ujumbe kwa Hezekia, akisema: Yawe, Mungu wa Israeli, anasema hivi: Kwa sababu umeniomba juu ya Saniharibu mufalme wa Asuria, basi huu ndio ujumbe wa Yawe juu ya huyo mufalme: Watu wa Sayuni wanakuzarau kabisa, Watu wa Yerusalema wanakutikisia kichwa kwa kukuchekelea. Wewe umemutukana nani? Umemutusi nani? Umesubutu kumufokea nani kwa majivuno? Ni Mungu, Mutakatifu wa Israeli! Umewatuma watumishi wako kumuchekelea Bwana wenu; wewe umesema: Kwa magari yangu mengi ya vita, nimefika juu kwenye vichwa vya milima, mpaka kwenye vichwa vya milima ya Lebanoni. Nimeangusha mierezi yake mirefu, na misunobari mizurimizuri. Nimevifikia vichwa vyake na ndani ya pori zake kubwa. Nimechimba visima na kunywa maji yake, na nilikausha vijito vya Misri kwa miguu yangu. Haujasikia, ewe Saniharibu, kwamba mimi Yawe nilipanga jambo hili tangu zamani? Ninachotimiza sasa nilikipanga zamani. Nilikuweka uifanye miji yenye kuzungukwa na kuta kuwa lundo la mabomoko. Wakaaji wake wakiwa wameishiwa nguvu, wametishika na kufazaika, wamekuwa kama mimea ya shamba, kama majani changa, kama majani yanayoota juu ya paa, yanayokauka mbele ya kukomaa. Lakini, ninakujua wewe Saniharibu; ninajua wakati unaikaa, wakati unatoka, na wakati unaingia; ninajua vilevile wakati kasirani yako inawaka juu yangu. Kwa vile umefanya mipango juu yangu na nimesikia majivuno yako, nitatia ndoana yangu ndani ya pua yako, na lijamu yangu ndani ya kinywa chako. Nitakurudisha katika njia ileile uliyokuja ndani yake. Na hiki ndicho kitakuwa kitambulisho kwako Hezekia: Mwaka huu na mwaka unaokuja mutakula kinachoota chenyewe bila kupandwa. Lakini katika mwaka wa tatu mutapanda na kuvuna mavuno; mutapanda mizabibu na kula matunda yake. Wale watakaobaki katika ukoo wa Yuda wataongezeka na kuwa wengi kama vile muti unavyotoa mizizi yake katika udongo na kuzaa matunda juu. Maana kutakuwa watu watakaobaki kule Yerusalema; kule kwenye mulima Sayuni kutakuwa watu wachache watakaobakia. Yawe wa majeshi amekusudia kukamilisha hayo. Yawe anasema hivi juu ya mufalme wa Asuria: Hataingia katika muji huu, wala kuupiga mushale, wala kuingia akishika ngao, wala hatalundika udongo kandokando yake apate kuubomoa. Basi, malaika wa Yawe aliingia ndani ya kambi ya Waasuria na kuwaua watu elfu mia moja makumi nane na watano. Kesho yake, wakati watu walipoamuka, waliona yale maiti yote. Kisha Saniharibu mufalme wa Asuria akaondoka, akaenda kwake, akakaa Ninawe. Siku moja, wakati Saniharibu alipokuwa akiabudu katika nyumba ya Nisiroki mungu wake, wana wake wawili, Adarameleki na Sarezeri, walimwua kwa upanga, halafu wakakimbilia katika inchi ya Ararati. Halafu mwana wake Esari-Hadoni akatawala kwa pahali pake. Wakati ule, Hezekia aligonjwa sana karibu kufa. Halafu nabii Isaya mwana wa Amozi akamwendea, akamwambia: Yawe anasema hivi: Panga mambo yako sawasawa katika nyumba yako kwa sababu utakufa, hautapona. Hezekia akageukia upande wa ukuta na kumwomba Yawe, akisema: Ee Yawe, ninakusihi ukumbuke jinsi nilivyokutumikia kwa uaminifu na kwa moyo wangu wote, na kutenda mazuri mbele yako. Hezekia akalia kwa uchungu sana. Kisha neno la Yawe lilimufikia Isaya kusema hivi: Kwenda umwambie Hezekia kwamba: Mungu wa baba yako Daudi, anasema hivi: Nimesikia ombi lako na nimeyaona machozi yako. Basi, ninakuongezea miaka kumi na mitano ya kuishi. Nitakuokoa wewe pamoja na muji huu toka katika mikono ya mufalme wa Asuria na kuulinda. Isaya akamujibu: Hiki kitakuwa kitambulisho kwako kutoka kwa Yawe kwamba Yawe atafanya kama alivyoahidi. Nitafanya kivuli kwenye daraja iliyojengwa na Ahazi, kirudi nyuma hatua kumi. Nacho kivuli kikarudi nyuma hatua kumi. Kisha mufalme Hezekia alipopona, akatunga wimbo huu wa shukrani: Nilisema: nikiwa mubichi kabisa, inanipasa niage dunia. Mimi nimepangiwa kwenda katika kuzimu siku zote zilizonibakilia. Nilisema sitamwona tena Yawe, katika inchi ya wanaokuwa wazima; wala sitamwona mutu yeyote tena, kati ya wakaaji wa ulimwengu. Makao yangu yameongolewa kwangu; kama hema la muchungaji; kama, mufumaji nimefika kwa mwisho wa kizingo cha maisha yangu; Mungu amekata nyuzi zinazokishika; hata mbele ya mwisho wa siku amenikomesha. Usiku kucha nililia kwa kuomba musaada; kama simba, anavunjavunja mifupa yangu; muchana na usiku ananikomesha. Ninalia kama mbaruwayi, ninaugua kama njiwa. Macho yangu yamefifia kwa kuangalia juu. Ee Bwana, ninateseka; ukuwe wewe usalama wangu! Lakini niseme nini: yeye mwenyewe aliniambia, naye mwenyewe ametenda hayo. Usingizi wangu wote umenitoroka kwa sababu ya uchungu ndani ya moyo wangu. Ee Bwana, sisi tunaishi kutokana na yote uliyotenda, kwa hayo yote mimi peke yangu vilevile ninaishi. Unirudishie afya, uniwezeshe kuishi. Nilipata mateso makali kwa faida yangu; lakini umeyaokoa maisha yangu kutoka shimo la uharibifu, maana umezitupa zambi zangu nyuma yako. Huko kuzimu mutu hawezi kukushukuru wewe; waliokufa hawawezi kukushukuru wewe. Wala wanaoshuka kule katika shimo hawawezi tena kutumainia uaminifu wako. Wanaokuwa wazima ndio wanaokushukuru, kama na mimi ninavyofanya leo. Wababa wanajulisha watoto wao uaminifu wako. Yawe ataniokoa. Nasi tutamusifu kwa nyimbo za vinubi siku zote za maisha yetu, katika nyumba ya Yawe. Isaya alikuwa amesema: Mutwae mukate wa tini na kuuweka kwenye jipu lake, apate kupona. Hezekia akauliza: Ni kitambulisho gani kitakachonijulisha kwamba mimi nitakwenda kwa nyumba ya Yawe? Wakati huo, mufalme Merodaki-Baladani mwana wa Baladani, mufalme wa Babeli, aliposikia kwamba Hezekia alikuwa mugonjwa na sasa amepona, alimutumia wajumbe waliomupelekea barua pamoja na zawadi. Basi, Hezekia aliwakaribisha na kuwaonyesha nyumba alimoweka mali yake: feza, zahabu, viungo vya kukoleza chakula, mafuta ya bei kali, vifaa vyake vyote vya vita na vitu vyote vilivyokuwa katika gala zake. Hakuna chochote katika nyumba yake ya kifalme au katika inchi yake ambacho hakuwaonyesha. Halafu nabii Isaya alikwenda kwa mufalme Hezekia na kumwuliza: Watu hawa wamesema nini? Na wametoka wapi? Naye Hezekia akamujibu: Wamekuja kutoka inchi ya mbali, kule Babeli. Halafu Isaya akamwuliza: Wameona nini katika nyumba yako ya kifalme? Hezekia akamujibu: Wameona yote yanayokuwa katika nyumba yangu ya kifalme. Hakuna chochote katika gala zangu ambacho sikuwaonyesha. Halafu Isaya akamwambia Hezekia: Sikia neno la Yawe wa majeshi: Siku zinakuja ambapo vyote vinavyokuwa katika nyumba yako na vitu vyote babu zako walivyokusanya mpaka leo, vitapelekwa Babeli. Hakuna kitu chochote kitakachobaki. –Ni Yawe anayesema hivyo.– Tena wamoja kati ya watoto wako wanaume watapelekwa, nao watakuwa matowashi watakaotumika katika nyumba ya mufalme wa Babeli. Naye Hezekia akamwambia Isaya: Neno la Yawe ulilosema ni zuri. Alisema hivyo maana alifikiri: Kutakuwa amani na salama muda wote wa maisha yangu. Mungu wenu anasema hivi: Muwafariji watu wangu. Muende kuwafariji. Museme na watu wa Yerusalema kwa upole, muwaambie kwamba utumwa wao umekwisha, wamesamehewa uovu wao. Yawe amewaazibu mara mbili kwa sababu ya zambi zao zote. Sauti inatangaza katika jangwa: Mutengenezee Yawe njia, munyooshe barabara kubwa kwa ajili ya Mungu wetu. Kila bonde litafunikwa, kila mulima na kilima vitasawanishwa; njia zenye lukumba zitanyooshwa, nazo zenye mashimo zitalainishwa. Kisha utukufu wa Yawe utafunuliwa, na watu wote pamoja watauona. Maneno haya yanatoka katika kinywa cha Yawe. Sauti inasema: Tangaza! Nami nikauliza: Nitangaze nini? Naye: Tangaza: wanadamu wote ni kama majani; usitawi wao ni kama maua ya shamba. Majani yananyauka na maua yanafifia, Yawe anapovumisha upepo juu yake. Hakika wanadamu ni kama majani. Majani yananyauka na maua yanafifia, lakini neno la Mungu wetu linadumu milele. Kwenda juu ya mulima murefu, ewe Sayuni, utangaze habari njema. Lalamika kwa nguvu, ewe Yerusalema, utangaze habari njema. Lalamika bila kuogopa. Uambie miji ya Yuda: Muangalie: Mungu wenu! Bwana wetu Yawe anakuja na nguvu, kwa mukono wake anatawala. Yeye anakuja na mapato yake, anafika na mushahara wake. Atachunga kundi lake kama muchungaji, atawakusanya wana-kondoo katika mikono yake, atawabeba kwa kifua chake, na atawaongoza polepole kondoo wanaonyonyesha. Ni nani anayeweza kupima maji ya bahari katika kitanga cha mukono wake, na kuzipima mbingu kwa mikono yake? Ni nani anayeweza kuutia udongo wa dunia katika kikombe; kuipima milima kwa mizani au vilima kwa kipimo cha uzito? Nani anayeweza kuiongoza akili ya Yawe, au kuwa mushauri wake na kumufundisha? Yawe alitaka shauri toka kwa nani, halafu akapata kuwa mwenye akili? Nani aliyemufundisha kuhukumu kwa haki? Nani aliyemufundisha maarifa, na kumwonyesha namna ya kuwa na akili? Kwake mataifa ni kama tone la maji katika mbeketi, ni kama mavumbi juu ya kilo. Kwake visanga ni vyepesi kama mavumbi laini. Kuni zote za Lebanoni na nyama wake wote havitoshi kwa sadaka ya kuteketezwa mbele yake. Mataifa yote si kitu mbele yake; kwake ni vitu vya ovyo na bure kabisa. Mutamulinganisha Mungu na nini basi, au ni kitu gani cha kumufananisha nacho? Anafanana na sanamu? Hiyo, fundi anaichonga, mufuaji wa zahabu anaipakaa zahabu, na kuitengenezea mukufu wa feza! Au ni sanamu ya muti mugumu? Hiyo ni kuni mutu anayochagua, akamutafuta fundi anayeelewa kazi, naye anamuchongea sanamu imara! Ninyi hamujui bado? Hamujapata kusikia? Hamukuambiwa tangu mwanzo? Hamujafahamu mwanzo wa dunia? Dunia iliumbwa na yule anayeikaa juu ya mbingu; kutoka huko wakaaji wa dunia ni kama mapanzi! Yeye ametandika mbingu kama pazia, na kuzikunjua kama hema la kuishi ndani yake. Yeye anawashusha wakubwa wenye nguvu, anawafanya watawala wa dunia kuwa si kitu. Mara tu wanaposimikwa na kuanza kuota, hata mbele hawajatoa mizizi kama miti katika udongo, Yawe akiwapulizia wananyauka, upepo mukali unawapeperusha kama makapi! Mungu Mutakatifu anauliza hivi: Basi, mutanilinganisha na nani? Kuna mutu anayeweza kuwa sawasawa mimi? Muinue macho yenu juu mbinguni! Ni nani aliyeziumba nyota hizo? Ni yule anayeziongoza kama jeshi lake, anayeijua hesabu yake yote, anayeziita kila moja kwa jina lake. Kwa sababu yeye ni mwenye nguvu nyingi, hakuna hata moja inayokosekana. Enyi watu wa Israeli wazao wa Yakobo, kwa nini munalalamika na kusema: Yawe hatujali sisi! Mungu wetu hajali haki yetu! Ninyi hamujui bado? Hamujapata kusikia? Yawe ndiye Mungu wa milele; yeye ndiye Muumba wa kila kitu katika dunia. Yeye haregei hata kidogo wala kuchoka. Maarifa yake hayachunguziki. Yeye anawapatia nguvu wanaokuwa zaifu, anawaongezea nguvu wale wanaoregea. Hata vijana wataregea na kuchoka; kweli washujaa wataanguka kwa muchoko. Lakini wote wanaomutumainia Yawe, watapata nguvu mupya. Watapanda juu kwa mabawa kama tai, watakimbia bila kuchoka, watatembea bila kuregea. Mungu anasema hivi: Enyi wakaaji wa mbali munyamaze munisikilize! Enyi mataifa mujitie moyo; mujitokeze na mujisemee, na mukuje tuende pamoja kwa hukumu. Ni nani aliyemwita shujaa toka mashariki, mutu ambaye anapata ushindi popote anapoenda? Mimi ninayaweka mataifa katika mikono yake, naye anawaponda wafalme chini ya miguu yake! Upanga wake unawafanya kuwa kama mavumbi, kwa upinde wake anawapeperusha kama maganda. Yeye anawakimbiza na kupita kwa usalama; anaenda mbio bila kukanyaga chini. Nani aliyefanya yote haya yatendeke? Ni nani aliyepanga wakati wa kila tukio? Mimi Yawe nipo tangu mwanzo, mimi nitakuwa hata milele. Wakaaji wa mbali wameona mambo niliyotenda, wakaogopa; dunia yote inatetemeka kwa woga. Watu wote wamekusanyika, wakakuja. Kila mumoja anamusaidia mwenzake akisema: Ujipe moyo! Fundi anamusaidia mufuaji wa zahabu. Naye anayelainisha sanamu kwa hama, anamusaidia anayeiunga kwa misumari. Wote wanasema: Ni vizuri sana! Kisha wanaifunga kwa misumari isitikisike. Sikiliza ewe Israeli, mutumishi wangu, wewe, Yakobo ambaye nimekuchagua, wewe wa uzao wa Abrahamu, rafiki yangu; wewe niliyekuleta toka miisho ya dunia, niliyekuita toka mbali kwa mipaka ya dunia, wewe niliyekuambia: Wewe ni mutumishi wangu; mimi sikukutupilia, lakini nilikuchagua. Basi, usiogope, mimi nipo pamoja nawe. Usifazaike, mimi ni Mungu wako. Nitakuimarisha na kukusaidia; nitakulinda kwa mukono wangu wa ushindi. Kweli! Wote waliokukasirikia, watapata haya na kufezeheka. Wote wanaopingana nawe, watakuwa wa bure na kuangamia. Utawatafuta hao wanaopingana nawe, hautawaona tena; wale wanaofanya vita nawe, watakuwa wameangamia. Mimi ndiye Yawe, Mungu wako, ndiye ninayeshika mukono wako. Mimi ndiye ninayekuambia: Usiogope, nitakusaidia. Enyi watu wa Yakobo zaifu kama mududu, enyi Waisraeli, musiogope! Nitawasaidia. –Ni ujumbe wa Yawe.– Mukombozi wenu ni yule Mutakatifu wa Israeli. Nitawafanya mukuwe kama chombo cha kupepeta, chenye meno mapya na makali. Mutaipepeta milima na kuipondaponda; mutavisagasaga vilima kama maganda. Mutaipepeta milima hiyo, nao upepo utaipeperushia mbali, zoruba itaitawanya huko na huko. Nanyi mutafurahi kwa sababu yangu Yawe; mutaona utukufu kwa sababu yangu Mungu Mutakatifu wa Israeli. Wamasikini na wakosefu wakitafuta maji lakini hawayapati, wakiwa wamekauka koo kwa kiu, mimi Yawe nitawajibu; mimi Mungu wa Israeli, sitawaacha. Nitabubujisha mito kwenye milima mitupu, na chemichemi katika mabonde. Nitaigeuza jangwa kuwa ziwa la maji, na inchi kuwa chemichemi za maji. Nitapanda miti kule katika jangwa: mierezi, mivinje, mijohoro, na mizeituni; nitaweka kule katika jangwa: miberoshi, shindano na misunobari. Watu wataona jambo hilo, nao watatambua na kuelewa kwamba mimi Yawe nimetenda hayo, mimi Mutakatifu wa Israeli nimefanya jambo hilo. Yawe, Mufalme wa Yakobo, anasema: Enyi miungu ya mataifa, mulete maneno yenu, mukuje mujitetee! Mujongee, mutuambie yatakayotukia. Mutuambie matukio ya kwanza yalikuwa gani, nasi tutafikiri juu yake. Au mututangazie jinsi yatakavyotimia, kusudi tujue yatakayokuja. Mutuambie yatakayotokea nyuma, nasi tujue basi kama ninyi ni miungu. Mufanye kitu chochote, chema au kibaya, kusudi tushangae na kuogopa. Hakika, ninyi si kitu kabisa. Hamuwezi kufanya kitu chochote. Anayechagua kuwaabudu ninyi ni chukizo. Nimetokeza mutu toka kaskazini, naye amekuja; nimemuchagua mutu toka mashariki, naye atalitaja jina langu. Yeye atawakanyaga wafalme kama matope, kama vile mufinyanzi anavyoponda udongo wake. Nani aliyetangaza haya tangu mwanzo, hata sisi tupate kuyatambua? Nani aliyetangulia kuyatangaza, kusudi sasa tuseme, alisema ukweli? Hakuna hata mumoja kati yenu aliyeyataja, wala hakuna aliyesikia maneno yenu. Mimi ni yule wa kwanza. Nilitangaza kwa Sayuni, nikapeleka Yerusalema mujumbe wa habari njema. Nimeangalia vizuri sana, lakini simwoni mutu yeyote; hakuna yeyote kati ya hao miungu anayeweza kushauri; nikiuliza, hakuna anayeweza kunijibu. Miungu hiyo yote ni udanganyifu, haiwezi kufanya kitu chochote; sanamu zao ni upepo tu, hazina maana. Muangalie mutumishi wangu ninayemusaidia; muchaguliwa wangu ambaye moyo wangu umependezwa naye. Nimeiweka roho yangu juu yake, naye ataimarisha sheria yangu katika mataifa. Hatalalamika wala hatapiga kelele, wala hatasema kwa sauti kubwa katika barabara. Hatavunja tete lililokunjama, hatazimisha utambi unaotoa moshi; ataimarisha sheria yangu kwa uaminifu. Yeye hataregea wala kuchoka, mpaka atakapoimarisha sheria yangu katika dunia. Watu wa mbali wanangojea mafundisho yake. Hivi ndivyo anavyosema Yawe aliyeumba mbingu na kuzitandika kama hema, aliyeifanya dunia na vyote vinavyokuwa ndani yake, anayewapa watu wanaokaa ndani yake uzima, na kuwajalia uzima wote wanaoishi ndani yake: Mimi Yawe nimekuita kutenda haki, nimekushika mukono na kukulinda. Kwa njia yako nitafanya ahadi na watu wote, wewe utakuwa mwangaza wa mataifa. Utayafungua macho ya vipofu, utawafungua wafungwa toka katika kifungo, utawaweka huru wale waliofungwa katika giza. Jina langu mimi ni Yawe; sitamupa mwingine utukufu wangu, wala sifa zangu sanamu za miungu. Mambo niliyotabiri yametukia; na sasa ninatangaza mambo mapya, ninakuelezea hayo mbele hayajatukia. Mumwimbie Yawe wimbo mupya! Dunia yote iimbe sifa zake: bahari na vyote vinavyokuwa ndani yake, inchi za mbali na wakaaji wake; jangwa na miji yake yote vipige kelele, vijiji vya wakaaji wa Kedari vimusifu, wakaaji wa Sela waimbe kwa shangwe; wapige kelele kutoka juu kwenye mulima. Wote wanaokaa katika inchi za mbali, wamutukuze na kumusifu Yawe. Yawe anajitokeza kama shujaa; kama vile askari katika vita anatatanua kupigana. Anapiga kelele kubwa la vita na kujionyesha mwenye nguvu juu ya waadui zake. Yawe anasema hivi: Kwa muda murefu sasa nimenyamaza, nimekaa kimya na kujizuiza; lakini sasa nitalia kama mwanamuke wakati wa kuzaa, anayeugua pamoja na kupumua kwa nguvu. Nitaharibu milima na vilima, na majani yote nitayakausha. Mito ya maji nitaigeuza kuwa inchi kavu, na visima vya maji nitavikausha. Nitawaongoza vipofu katika njia wasiyoifahamu, nitawaongoza katika njia ambazo hawazijui. Mbele yao nitaligeuza giza kuwa mwangaza, na pahali penye kuharibika patakuwa laini. Huo ndio mupango wangu wa kufanya, nami nitautimiza. Wote wanaotegemea sanamu za miungu, wote wanaoziambia “Ninyi ni miungu yetu” watakomeshwa na kupata haya. Musikilize enyi viziwi! Muangalie, enyi vipofu, mupate kuona! Nani anayekuwa kipofu isipokuwa mutumishi wangu? Nani anayekuwa kiziwi kama mujumbe ninayemutuma? Ni nani anayekuwa kipofu kama huyu niliyemutakasa, au kipofu kama mutumishi wa Yawe? Ninyi mumeona mambo mengi, lakini hamuelewi kitu. Masikio yenu yako wazi, lakini hamusikii kitu! Kwa ajili ya uaminifu wake, Yawe, alipenda kutukuza sheria yake na kuiheshimisha. Lakini hawa ni watu walioibwa mali yao na kunyanganywa! Wote wamenaswa katika mashimo, wamefungwa katika kifungo. Wamenyanganywa bila mutu wa kuwaokoa, wamekamatwa mateka na hakuna anayesema: Muwarudishe! Mutatega masikio kwa kusikia kitu hiki? Nani kati yenu atakayesikiliza vizuri yatakayotukia? Ni nani aliyewatia Waisraeli katika mikono ya waadui zao? Nani aliyewaacha wanyanganywe mali zao? Ni Yawe ambaye tumemukosea! Wazee wetu walikataa kuzifuata njia zake, wala hawakuzitii amri zake. Kwa hiyo aliwamwangia kasirani yake kali, akawaacha kupatwa na vita kali. Hasira yake iliwawakia kila upande, lakini wao hawakuelewa chochote; iliwachoma, lakini hawakufikiri juu ya jambo hilo. Yawe aliyewaumba enyi watu wa Yakobo, yeye aliyewafanya enyi watu wa Israeli, anasema hivi: Musiogope, maana mimi nimewakomboa; nimewaita kwa jina lenu nanyi ni wangu. Mukipita katika maji, mimi nitakuwa pamoja nanyi; mukipita katika mito, haitawashinda nguvu. Mukitembea katika moto, hamutaungua; ulimi wa moto hautawaunguza. Maana mimi ni Yawe, Mungu wenu, Mungu Mutakatifu wa Israeli, Mwokozi wenu. Ninaitoa inchi ya Misri kwa ajili ya ukombozi wenu, ninaitoa Kushi na Seba kusudi muachwe huru. Ninyi ni wa bei kali mbele yangu, ninawaheshimu na kuwapenda. Kwa hiyo, ninatoa watu kusudi niwapate ninyi, ninayaachilia mataifa pahali pa maisha yenu. Musiogope maana mimi nipo pamoja nanyi. Nitawarudisha wazao wenu toka mashariki, nitawakusanya ninyi kutoka magaribi. Nitaiambia kaskazini: “Uwaache waondoke”, na kusini: “Usiwazuize! Muwarudishe watu kutoka mbali, kutoka kila pahali katika dunia. Kila mumoja anajulikana kwa jina langu; niliwaumba wote na kuwafanya kwa ajili ya utukufu wangu.” Muwalete mbele watu hao, ambao wana macho lakini hawaoni, wana masikio lakini hawasikii! Mataifa yote yakusanyike, watu wote wakutane pamoja. Nani kati ya miungu yao anayeweza kutangaza yatakayotukia? Nani anayeweza kutuonyesha yanayotukia sasa? Wawalete washuhuda wao, kuhakikisha kwamba walifanya hivyo. Uwaache wasikilize na kusema: Ilikuwa kweli. Ninyi Waisraeli ni washuhuda wangu. –Ni ujumbe wa Yawe.– Niliwachagua mukuwe watumishi wangu, mupate kunijua na kuniamini, kwamba mimi ni Mungu. Mbele yangu hakukuwa mungu mwingine, wala hakutakuwa mungu mwingine nyuma yangu. Mimi peke yangu ndiye Yawe, hakuna mukombozi mwingine isipokuwa mimi. Nilitangaza yale ambayo yangetukia, kisha nikakuja na kuwakomboa. Hakuna mungu mwingine aliyetangulia kufanya hivyo, nanyi ni washuhuda wangu. –Ni ujumbe wa Yawe.– Mimi ni Mungu na nitakuwa Mungu siku zote. Hakuna anayeweza kuepuka nguvu yangu; hakuna anayeweza kupinga ninayofanya. Yawe, Mukombozi wenu, Mutakatifu wa Israeli, anasema hivi: Kwa ajili yenu nitatuma waaskari kwenda Babeli. Nitavunja vifungio vya milango ya muji wake, na kelele za wale Wakaldea zitageuka maombolezo. Mimi ni Yawe, Mutakatifu wenu; Mimi ndiye Muumba wa Israeli, Mufalme wenu. Musiyakumbuke mambo yaliyopita, wala musifikiri juu ya vitu vya zamani. Muangalie, mimi ninafanya kitu kipya. Kinafanyika sasa hivi, nanyi mutaweza kukiona. Nitafanya njia katika mbuga, na kububujisha mito katika jangwa. Nyama wa pori wataniheshimu, mbweha na mbuni, maana nitaweka maji katika mbuga, na kububujisha mito katika jangwa, kwa kuwakunywesha watu wangu niliojichagulia, watu niliowaumba kwa ajili yangu mwenyewe, kusudi wazitangaze sifa zangu! Lakini ewe taifa la Yakobo, haukuniabudu mimi; enyi watu wa Israeli, mulichoka nami! Hamujaniletea kondoo wenu wa sadaka za kuteketezwa, wala kuniheshimu kwa sadaka zenu. Nami sikuwalemea ninyi kwa kutaka sadaka, wala sikuwachokesha kwa kuwadai ubani. Hamukuninunulia marasi kwa mali yenu, wala kunishibisha kwa mafuta za sadaka. Pahali pake zambi zenu zimekuwa muzigo kwangu, mumenichokesha kabisa kwa makosa yenu. Lakini mimi ndiye niliyefuta makosa yenu kwa heshima yangu, ndiye ninayefuta makosa kwa ajili yangu mwenyewe, wala sitazikumbuka zambi zenu. Munikumbushe tena makosa yangu, tusambe nanyi, mutoe mashitaki yenu kusudi tuuone ukweli wenu! Babu yenu wa kwanza alitenda zambi, wapatanishi wenu waliniasi. Kwa hiyo niliwazaraulisha wakubwa wa Pahali Patakatifu nikawaacha watu wa Yakobo waangamizwe, nikawaacha Waisraeli watukaniwe. Sikiliza, ewe Israeli, mutumishi wangu; sikiliza, enyi wazao wa Yakobo, muchaguliwa wangu. Mimi, Yawe Muumba wako, niliyekutengeza tangia tumbo la mama yako, ninakuja kukusaidia wewe. Mimi Yawe ninasema hivi: Musiogope, enyi wazao wa Yakobo, mutumishi wangu, usiogope, ewe Yeshuruni, muchaguliwa wangu. Nitaimwangilia maji inchi yenye kiu, na kutiririsha muto katika inchi iliyokauka. Nitajaza roho wangu juu ya wazao wako, nitawamwangia watoto wako baraka yangu. Watachipuka kama nyasi penye maji mengi, kama majani kandokando ya vijito. Mumoja atasema: “Mimi ni wa Yawe”, mwingine atajiita kwa jina la Yakobo, mwingine ataandika juu ya mukono wake: “Wa Yawe”, na kujitambulisha kwa jina la Israeli. Yawe, Mufalme na Mukombozi wa Israeli, Yawe wa majeshi anasema hivi: Mimi ni wa kwanza na wa mwisho; hakuna mungu mwingine isipokuwa mimi. Ni nani mungu anayekuwa kama mimi? Muache atangaze na kusema wazi mbele yangu. Nani alitangaza hapo zamani mambo ambayo yatatukia? Watuambie yale ambayo bado yatatokea. Enyi watu wangu, musiogope wala musikuwe na hofu, Sikuwaambia tangu zamani mambo yatakayotokea? Ninyi ni washuhuda wangu. Kuna mungu mwingine isipokuwa mimi? Kuna mwenye nguvu mwingine? Yule simujui! Watu wote wanaotengeneza sanamu za miungu ni bure kabisa; na vitu hivyo wanavyovifurahia haviwafalii kitu chochote. Wanaoshuhudia hiyo miungu ya uongo ni vipofu na wajinga. Kwa hiyo hao watafezeheshwa! Kuna faida gani kwa mutu kujitengenezea mungu au sanamu ya miungu? Hakika wote wanaoshirikiana na sanamu watapata haya, tena hao wafundi wa sanamu ni wanadamu tu. Basi, wakutane wote, wajitokeze, nao wataogopa na kufezeheka. Mufuaji wa vyuma anatwaa kipande cha chuma, anakiyeyusha kwa moto na kufua sanamu. Anakipondaponda na nyundo kusudi akipatie umbo kwa mikono yake yenye nguvu. Wakati wote huo yeye anasikia njaa na kuchoka; anasikia kiu na nguvu kuregea. Vilevile muchoraji wa miti anafanya vipimo vyake kwa kamba, anachapa kitambulisho chake, kisha anatumia vifaa vyake kwa kuchonga. Halafu anatengeneza sanamu na kuipatia umbo la mutu na sura ya kupendeza; kisha anaweka sanamu hiyo ya mungu pahali pake pa pekee. Mutu anakata muti wa mwerezi kusudi autumie, au anachagua muvula au mwalo. Anauacha ukomae kati ya miti ya pori. Au anaupanda mwerezi na mvua inaustawisha. Sehemu ya muti huo itatumiwa kama kuni; mutu anaota moto wake na kuchoma mikate yake juu yake. Sehemu nyingine ya muti huohuo, mutu anajichongea mungu na kumwabudu; anajitengenezea sanamu ya mungu na kupiga magoti mbele yake. Kisha anatwaa kuni zake, anakonga nazo moto, anachoma nyama juu yake, anaikula, na kushiba. Halafu anakaa pale akiota moto na kusema: Aa, kweli nimepata joto! Huo ndio moto! Sehemu iliyobaki ya muti huohuo, anajichongea nayo mungu, anajifanyia sanamu yake, kisha anapiga magoti mbele yake na kuiabudu. Wanaomba mbele yake wakisema: Wewe ni mungu wangu, uniokoe! Watu hao hawajui wala hawaelewi kitu chochote. Wamefungwa macho wasipate kuona na akili wasipate kufahamu. Hakuna anayeweza kuwaza au kuwa na akili na kufikiri na kusema: Kipande cha muti huo nilikikonga moto; tena nikachoma mikate juu ya makaa yake, nikachoma nyama, nikakula. Basi, sehemu iliyobaki namna gani nitatengeneza nayo sanamu ambayo ni chukizo na kuabudu hicho kipande cha muti? Hapana! Mawazo yao yameambatana na hicho ambacho ni majivu tu! Mutu huyo amepotoka hata hawezi kujiokoa mwenyewe na kusema: Kweli, hiki ninachokuwa nacho katika mukono wangu ni udanganyifu mutupu! Yawe anasema hivi: Ewe Israeli, watu wa Yakobo, kumbuka kwamba wewe ni mutumishi wangu. Nilikuumba kusudi ukuwe mutumishi wangu, nami sitakusahau hata kidogo. Nimezimisha makosa yako nayo yametoweka kama mawingu, nimefuta zambi zako, nazo zimepotea kama kunguku. Urudi kwangu maana mimi nimekukomboa. Muimbe kwa furaha enyi mbingu, kwa sababu ya yale Yawe aliyotenda. Mupige kelele enyi vilindi vya dunia! Mupige vigelegele enyi milima! Enyi mapori na miti yote inayokuwa ndani yake, mushangilie. Maana Yawe amewakomboa wazao wa Yakobo, naye atatukuzwa katika inchi ya Israeli. Yawe, Mukombozi wako, aliyekuumba tangu katika tumbo, anasema hivi: Mimi ndiye Yawe niliyeumba vitu vyote. Mimi peke yangu nilizitandaza mbingu, niliiumba dunia kwa nguvu yangu mwenyewe! Mimi ninavuruga maono ya manabii wa uongo na ninapoteza akili za waaguzi. Mimi ninayapinga maneno ya wenye hekima na kufanya elimu yao kuwa upumbafu. Lakini ninahakikisha ujumbe wa mutumishi wangu, na kukamilisha mipango ya wajumbe wangu. Mimi ndiye ninayesema juu ya Yerusalema: Wewe Yerusalema, watu watakaa ndani yako tena. Na juu ya miji ya Yuda: Ninyi mutajengwa tena: mabomoko yenu yatatengenezwa tena. Mimi ndiye ninayeviamuru vilindi: Mukauke, nitakausha mito yenu. Ndimi ninasema juu ya mufalme Kiro: Ni muchungaji niliyemuchagua kwa ajili yangu. Yeye atatimiza mipango yangu yote. Ndimi ninayesema juu ya Yerusalema: Wewe Yerusalema utajengwa tena upya; na juu ya hekalu: Musingi wako utawekwa tena. Yawe anasema hivi kwa Kiro, muchaguliwa wake: Nilikuchagua kuwa mufalme kwa kunitumikia. Ninaimarisha nguvu yako kusudi uyashinde mataifa mbele yako, na kuzivunja nguvu za wafalme. Mimi ninafungua milango ya muji mbele yako, na hakuna mulango utakaofungwa. Mimi nitakutangulia, na kuisawanisha milima mbele yako. Nitaivunjavunja milango ya shaba, na kuvikatakata vifungio vyake vya chuma. Nitakupa akiba zilizofichwa na mali inayokuwa pahali pa siri, upate kutambua kwamba mimi ni Yawe, Mungu wa Israeli, ninayekuita kwa jina lako. Kwa ajili ya mutumishi wangu Yakobo, muchaguliwa wangu Israeli, nimekuita kwa jina lako; nimekupa jina la heshima ingawa wewe haunijui. Mimi ni Yawe, wala hakuna mwingine; hakuna Mungu mwingine lakini mimi. Ninakuimarisha ingawa wewe haunijui, kusudi watu wote, toka mashariki mpaka magaribi, wajue kwamba hakuna Mungu mwingine isipokuwa mimi tu. Mimi ni Yawe na hakuna mwingine. Mimi ninafanya mwangaza na kuumba giza; ninaleta uheri na kusababisha hasara. Mimi Yawe ninatenda vitu hivi vyote. Enyi mbingu, munyeshe umande kutoka kule juu, mawingu yatiririshe ushindi; dunia ifuguke, ichipushe wokovu, na kuotesha haki vilevile! Mimi, Yawe nimefanya hayo. Ole kwake mutu anayebishana na Muumba wake: chombo cha udongo kubishana na mufinyanzi wake! Udongo unamwuliza anayeufinyanga: Unatengeneza nini hapa? au kumwambia: Kazi yako si kamili! Ole kwake mutu anayemwambia baba: Umezaa nini? au anayemwambia mama: Umeleta nini katika dunia? Yawe, Mutakatifu wa Israeli, Mungu, Muumba wa Israeli anasema hivi: Munataka kuniuliza juu ya watoto wangu, au kuniamuru juu ya kazi zangu mwenyewe? Ni mimi niliyeifanya dunia, na kuumba mwanadamu anayeishi humo. Mikono yangu ndiyo iliyozitandaza mbingu, na kundi lote la nyota liko kwa amri yangu. Ni mimi niliyemwamuru Kiro akuje, atimize mapenzi yangu. Nitazifanikisha njia zake zote. Ataujenga upya muji wangu Yerusalema, na kuwapa uhuru watu wangu wanaokuwa katika uhamisho, bila kutaka malipo wala zawadi. –Ni Yawe wa majeshi anayesema hivyo. Yawe anasema hivi: Utajiri wa Misri na faida ya uchuuzi za Kushi, pamoja na za watu wa Seba, wale watu warefu sana, zitakuja kwako mwenyewe wewe taifa la Israeli, zote zitakuwa mali yako. Watu hao watakufuata wakifungwa minyororo; watainama mbele yako na kukusihi wakisema: Kwako kuna Mungu wa kweli, wala hakuna Mungu mwingine lakini yeye. Kweli wewe ni Mungu mwenye kufichama, Mungu wa Israeli, Mungu mwokozi. Watengenezaji wa sanamu watapata haya na kuzarauliwa, wote pamoja watafezeheka. Lakini taifa la Israeli litaokolewa na Yawe, litapata wokovu wa milele. Halitapata haya wala kuzarauliwa milele. Hivi ndivyo anavyosema Yawe aliyeumba mbingu, ndiye Mungu aliyeipa dunia umbo na kuifanya na kuiimarisha. Hakuiumba kusudi ibaki ukiwa, lakini aliipa umbo kusudi iikaliwe na viumbe vyake: Mimi ni Yawe, wala hakuna mwingine. Mimi sikusema kwa siri, wala katika inchi yenye giza. Mimi sikuwaambia wazao wa Yakobo wanitafute pahali kusipokuwa kitu. Mimi Yawe ninasema ukweli, maneno yangu ni ya kuaminika. Enyi watu wa mataifa muliobaki, mukusanyike pamoja mukuje! Ninyi mumekosa akili: ninyi munabeba sanamu za miti na kumwomba mungu asiyeweza kuokoa watu. Mutangaze na kusema habari zenu. Mufanye shauri pamoja! Ni nani aliyetangaza zamani matukio ya sasa? Ni nani aliyesema mambo haya zamani? Haikukuwa mimi Yawe? Hakuna Mungu mwingine isipokuwa mimi! Mimi ni Mungu wa haki na mwokozi; hakuna mwingine isipokuwa mimi. Munigeukie mimi mupate kuokolewa, popote munapokuwa katika dunia. Maana mimi ni Mungu, wala hakuna mwingine. Mimi nimeapa kwa nafsi yangu, ninachosema ni ukweli, neno langu halitarudi nyuma: kila mwanadamu atanipigia magoti, kila mutu atafanya kiapo. Watasema juu yangu: Haki na nguvu viko kwa Yawe peke yake. Wote waliomukasirikia Yawe watakuja kwake na haya. Lakini wazao wa Israeli watapata ushindi toka kwa Yawe na kufurahi. Ule mungu Bali ameanguka; mungu Nebo anainama. Sanamu zao zinabebwa juu ya nyama, juu ya nyama wanaobeba mizigo! Vitu ninyi mulivyokuwa mukiviinua juu, vinakuwa sasa mizigo, vinakuwa mizigo mizito juu ya nyama wenye kuchoka. Wanajiinamisha, wanainama pamoja. Hawakuweza kuziokoa sanamu zao. Wao wenyewe vilevile wamepelekwa katika utumwa! Musikilize, enyi wazao wa Yakobo, munisikilize, enyi mabaki ya watu wangu wa Israeli. Mimi niliwatunza ninyi tangu mulipozaliwa; niliwabeba ninyi tangu katika tumbo la mama yenu. Mimi nitabaki yuleyule hata katika uzee wenu; hata katika wakati wenu wa imvi mimi nitawabeba. Nilifanya hivyo kwanza, nitafanya hivyo tena. Nitawabeba ninyi na kuwaokoa. Mutanifananisha na nani na kunisawanisha naye? Mutanilinganisha na nani nipate kuwa sawasawa naye? Watu wanapoteza zahabu kutoka mifuko yao, wanapima feza kwenye mizani zao, wanamulipa mufuaji wa zahabu awatengenezee sanamu ya mungu, kisha wanainama mbele yake na kuiabudu! Wanajibebesha sanamu hiyo juu ya mabega na kuipeleka, kisha wanaiweka pahali pake, nayo inakaa palepale; haiwezi hata kidogo kusogea kutoka pale inapokuwa. Mutu akiililia, haiwezi kumwitikia, wala haiwezi kumwokoa mutu katika taabu zake. Mukumbuke jambo hili na kufikiri, mujiulize ndani ya mioyo yenu enyi waasi. Mukumbuke mambo niliyotenda hapo zamani! Mimi ni Mungu. Hakuna Mungu mwingine. Mimi ni Mungu. Hakuna mwingine kama mimi. Nilitangaza mambo ya mwisho tangu mwanzo, tangu zamani nilitangaza mambo yatakayotukia. Kusudio langu litatimia; mimi nitatimiza nia yangu yote. Ninamwita tai wangu kutoka mashariki, ambaye atatimiza kusudi langu toka inchi ya mbali. Mimi nimesema na nitafanya; mimi nimepanga nami nitatimiza. Musikilize, enyi wenye vichwa vigumu, munisikilize enyi munaokuwa mbali na ukombozi. Siku ya kuwakomboa inakaribia, haiko mbali tena; siku ya kuwaokoa ninyi haitachelewa. Nitauokoa Sayuni, nitaleta utukufu kwa Israeli. Shuka, uikae katika mavumbi, ewe bikira, binti wa Babeli! Ikaa chini pasipo kiti cha kifalme, ewe binti wa Wakaldea! Tokea sasa hautaitwa tena murembo wala mwenye kupendeza. Utwae mawe ya kusagia, usage unga kama mutumwa! Vua kitambaa chako, pandisha kanzu yako! Onyesha miguu yako kwa kuvuka mito. Watu watauona uchi wako; wataona haya yako. Mimi nitalipiza kisasi, wala sitamuhurumia mutu yeyote. Mukombozi wetu ndiye Mutakatifu wa Israeli; Yawe wa majeshi ndilo jina lake. Ikaa kimya, ingia katika giza, ewe taifa la Wakaldea. Maana umepoteza cheo yako ya kuwa malkia wa falme. Niliwakasirikia watu wangu, Israeli, nikawafanya watu wangu kuwa wanaharamu. Niliwatia katika mikono yako, nawe haukuwaonea huruma; na wazee uliwabebesha nira nzito sana. Ulijisemesha ndani ya moyo: “Nitakuwa malkia milele”, nawe haukufikiri juu ya mambo yanayotokea, wala kuwaza juu ya mwisho wake. Sasa, basi, sikiliza, ewe mupenda raha, wewe unayezani kuwa katika usalama, na kujisemesha: Mimi ndiye. Hakuna mwingine isipokuwa mimi. Sitakuwa mujane hata kidogo, wala sitakufiwa na watoto wangu. Haya yote mawili yatakupata kwa rafla katika siku moja: kupoteza watoto wako na kuwa mujane, ijapokuwa una wingi wa uchawi wako, na nguvu nyingi za uganga wako. Ulijiona salama katika uovu wako; ukajisemesha: Hakuna mutu anayeniona. Hekima na elimu yako vilikupotosha, ukajisemesha ndani ya moyo wako: Mimi ndiye; hakuna mwingine isipokuwa mimi. Lakini hasara itakupata ambayo hautaweza kujiepusha nayo. Magumu yatakutokea ambayo hautaweza kuyapinga; maangamizi yatakufikia kwa rafla ambayo haujapata kuyaona hata kidogo. Endelea basi na uganga wako, tegemea wingi wa uchawi wako. Wewe uliyashugulikia tangu ujana wako ukitumainia kwamba utafanikiwa au kusababisha woga kwa watu! Wewe umejichokesha bure na washauri wako. Basi, wajitokeze hao wenye akili wakuokoe! Wao wanagawanya mbingu sehemusehemu, wanachunguza nyota na kutabiri kila mwezi yatakayokupata. Wao ni kama majani yenye kukauka: moto utayateketeza! Hawawezi hata kujiokoa wenyewe mbali na ukali wa moto huo. Moto huo si wa kujipatia joto, huo si moto wa kuota! Ndivyo watakavyokuwa hao uliowategemea hivyo, hao uliojishugulisha nao tangu ujana wako. Watatangatanga kila mumoja njia yake; hakuna hata mumoja atakayeweza kukuokoa. Musikilize, enyi watu wa Yakobo, enyi munaojulikana kwa jina la Israeli, ninyi munaokuwa wa uzao wa Yuda. Ninyi munaapa kwa jina la Yawe, na kudai kwamba munamwabudu Mungu wa Israeli; lakini hayo si ukweli wala sawa. Ninyi munaona utukufu kujiita watu wa muji mutakatifu, na kujidai kumutegemea Mungu wa Israeli, ambaye jina lake ni Yawe wa majeshi. Nilitangaza zamani matukio ya mbele, niliyatangaza mimi mwenyewe na kuyafanya yajulikane kwenu. Mara moja nikaanza kuyatimiza, nayo yakapata kutukia. Lakini nilikujua wewe kuwa na moyo mugumu; kichwa kigumu kama chuma, uso wako kama shaba. Kwa hiyo nilikutangazia mambo yale tangu zamani, mbele hayajatukia, mimi nilikujulisha, kusudi usiseme: Ni sanamu yangu iliyotenda mambo hayo, sanamu zangu za chuma ndizo ziliyaagiza. Wewe uliyasikia na sasa unayaona yote. Kwa nini hauwezi kuyakubali? Tangu sasa nitakujulisha mambo mapya; mambo yaliyofichwa ambayo haukuyajua. Mambo hayo yanatukia sasa; haukupata kuyasikia mbele ya siku ya leo, hivyo hauwezi kusema: Aa! Nilikwisha kuyajua. Haujapata kuyasikia wala kuyajua hata kidogo; tangu zamani masikio yako hayakuyasikia. Nilijua kwamba wewe ni mudanganyifu, na kwamba wewe ni mwasi tangu kuzaliwa. Kwa heshima ya jina langu, ninatuliza hasira yangu; kwa ajili ya heshima yangu, ninajizuiza kusudi nisikuangamize. Mimi nimekusafisha lakini si kama feza katika furu. Nimewapima katika furu ya taabu. Ninafanya hivyo kwa ajili yangu mwenyewe. Kwa nini jina langu lizarauliwe? Siwezi kumupatia mwingine utukufu wangu! Unisikilize ee taifa la Yakobo, unisikilize ee Israeli niliyekuita. Mimi ndiye. Mimi ni wa kwanza na wa mwisho. Kwa mukono wangu niliuweka musingi wa dunia, mimi mwenyewe nilizitandaza mbingu. Nikiziita mbingu na dunia, zinasimama haraka mbele yangu. Mukusanyike wote musikilize! Nani kati yenu alitabiri vitu hivi? Yule ambaye Yawe anamupenda atatimiza mapenzi yake juu ya Babeli, atawashambulia Wakaldea. Mimi –ni mimi!– nimesema na kumwita; nimemuleta, naye atafanikiwa katika mupango wake. Musogee karibu nami musikie jambo hili: Tangu mwanzo mimi sikusema kwa siri, tangu mambo hayo yaanze kutendeka, nimekuwa pale. Sasa, Bwana wetu Yawe amenituma, na kunipa nguvu ya Roho wake. Yawe, Mutakatifu wa Israeli, Mukombozi wako, anasema hivi: Mimi ndiye Yawe, Mungu wako; ninayekufundisha kwa faida yako na kukuongoza katika njia unayotakiwa kwenda. Ingekuwa heri ungalizitii amri zangu! Halafu baraka zingekutiririkia kama muto, ungefanikiwa kwa wingi kama mawimbi ya bahari. Wazao wako wangekuwa wengi kama muchanga, kama chembe za muchanga. Jina lao lisingalisahauliwa hata kidogo, wala halingalifutwa mbele yangu. Sasa, muondoke Babeli! Mukimbie kutoka kwa Wakaldea! Mutangaze jambo hili kwa sauti za shangwe. Mueneze habari zake kila pahali katika dunia. Museme: Yawe amekomboa taifa la mutumishi wake Yakobo. Alipowaongoza katika jangwa hawakuona kiu, aliwatiririshia maji kutoka katika jiwe, alipasua jiwe maji yakabubujika. Lakini Yawe anasema hivi: Hakuna amani kwa watu waovu. Munisikilize, enyi inchi za mbali, Mutege sikio, enyi watu wa mbali! Yawe aliniita mbele sijazaliwa, alitaja jina langu nikiwa katika tumbo la mama yangu. Alifanya maneno yangu kuwa makali kama upanga mukali, alinificha katika kivuli cha mukono wake; aliufanya ujumbe wangu kuwa mukali kama chongo ya mushale, akanificha kama mushale ndani ya mufuko wake. Aliniambia: Wewe ni mutumishi wangu; kwa njia yako, ee Israeli, watu watanitukuza. Lakini mimi nikafikiri: Nimeshugulika bure, nimetumia nguvu zangu bure kabisa. Hata hivyo, Yawe atanipa haki yangu; mushahara wa kazi yangu uko kwa Mungu. Lakini sasa Yawe anasema. Aliniita tangu katika tumbo la mama kusudi nipate kuwa mutumishi wake, nilirudishe taifa la Yakobo kwake na kukusanya wazao wa Israeli kwake. Yawe amenijalia heshima mbele yake. Mungu wangu amekuwa nguvu yangu. Yeye anasema: Haitoshi tu wewe kuwa mutumishi wangu, kusudi uyainue makabila ya Yakobo, na kurudisha watu wa Israeli waliobaki. Nitakufanya ukuwe mwangaza wa mataifa, kusudi watu wote wapate kuokolewa katika dunia. Yawe, Mukombozi na Mutakatifu wa Israeli, anamwambia hivi yule anayezarauliwa sana, yule anayechukiwa na mataifa, na ambaye ni mutumishi wa watawala: Wafalme wataona nao watasimama; wakubwa watainama na kuabudu kwa heshima ya Yawe ambaye anatimiza ahadi zake, kwa heshima ya Mutakatifu wa Israeli ambaye amekuchagua wewe. Yawe anasema hivi: Wakati uliofaa nilijibu maombi yako; wakati wa wokovu nilikusaidia. Nimekuweka na kukufanya ukuwe kiungo cha agano langu na mataifa yote: utatengeneza inchi na kurudisha tena inchi hiyo iliyoharibika. Utawaambia wafungwa: Mutoke humo katika kifungo na wale wanaokuwa katika giza: Mukuje inje kwenye mwangaza! Kila pahali watakapokwenda watapata chakula hata kwenye vilima vitupu watapata malisho. Hawatasikia tena njaa wala kuwa na kiu. Upepo wenye kuunguza wala jua havitawachoma, mimi niliyewahurumia nitawaongoza na kuwapeleka kwenye chemichemi za maji. Milima yote nitaifanya kuwa njia, na barabara zangu kubwa nitazitengeneza. Watu wangu watarudia kutoka mbali, wengine kutoka kaskazini na magaribi, wengine kutoka upande wa kusini. Muimbe kwa furaha, enyi mbingu! Ushangilie ewe dunia, Enyi milima, mulalamike kwa furaha, maana Yawe amewafariji watu wake, anawaonea huruma watu wake wanaoteseka. Wewe Sayuni unasema: Yawe ameniacha. Hakika Bwana wangu amenisahau. Lakini Yawe anasema: Munafikiri kwamba mama anaweza kumusahau mutoto anayemunyonyesha, wala kumuchukia mutoto wa tumbo lake? Hata kama mama anaweza kumusahau mutoto wake, mimi sitakusahau hata kidogo. Nimekuchora wewe katika vitanga vya mikono yangu; kuta zako ninaziona mbele yangu siku zote. Watakaokujenga upya wanakuja haraka, wale waliokuharibu wanaondoka. Inua macho uangalie pande zote; watu wako wote wanakusanyika na kukufikia. Kama vile ninavyoishi, watu wako watakuwa kwako kama mapambo, utawafurahia kama vile bibi arusi anavyofanya na taji lake. –Ni ujumbe wa Yawe. Kweli umepatwa na uharibifu, makao yako yamekuwa matupu, na inchi yako imeteketezwa. Lakini sasa itakuwa ndogo sana kwa wakaaji wake. Watoto wako waliozaliwa katika uhamisho, watakulalamikia wakisema: Inchi hii ni ndogo sana; utupatie nafasi zaidi ya kuishi. Kwa hiyo utajiuliza mwenyewe: Nani aliyenizalia watoto hawa wote? Nilikufiwa na watoto bila kupata wengine. Nilipelekwa katika uhamisho na kutupwa mbali; nani basi aliyewalea watoto hawa? Mimi niliachwa peke yangu, sasa, hawa wametoka wapi? Bwana wetu Yawe anasema hivi: Nitasimika bendera kwa kuita mataifa; nitayaonyesha kitambulisho. Nayo yatawarudishia wana wenu wakiwabeba kwenye kifua, vilevile na wabinti zenu kwenye mabega. Wafalme watakushugulikia, na malkia watakutengenezea chakula. Watainama mbele yako uso mpaka chini, na kulambula mavumbi ya miguu yako. Halafu utatambua kwamba mimi ni Yawe; wote wanaonitegemea hawatapata haya. Watu wa Yerusalema wanalalamika: Shujaa, anaweza kunyanganywa vitu alivyoteka? Au wafungwa wa mutu mutesaji wanaweza kuokolewa? Yawe anasema hivi: Kweli! Hata mateka za shujaa zitarudishwa, wafungwa wa mutu mutesaji wataokolewa. Mimi mwenyewe nitawapiganisha waadui zako, mimi mwenyewe nitawaokoa watoto wako. Nitawasukuma watesaji wako wakule miili yao wenyewe; watalewa damu yao wenyewe kama divai. Halafu wanadamu wote watatambua kwamba mimi ni Yawe, Mwokozi wako, Mukombozi wako, Mwenye Nguvu wa Yakobo. Yawe anasema hivi: Kama nimeachana na mama yako Yerusalema, barua ya kuachana iko wapi? Nilikuwa na deni ya nani kwa kuwauzisha? Mukumbuke kwamba muliuzishwa kwa ajili ya maovu yenu, mama yenu alifukuzwa kwa ajili ya makosa yenu. Nilipokuja, kwa nini sikukuta mutu? Nilipoita mbona hamukuitikia? Mukono wangu ni mufupi hata nisiweze kuwaokoa ninyi? Sina nguvu ya kuwakomboa? Ninakausha bahari kwa kuikaripia, na mito ninaifanya kuwa jangwa; samaki wake wanakufa na kunuka kwa kukosa maji. Mimi ninafunika anga kwa giza, na kulivalisha nguo ya kilio. Bwana wetu Yawe amenifundisha jinsi ya kusema, kusudi niwatie moyo wale waliochoka. Kila asubui ananipa hamu ya kusikiliza mambo anayotaka kunifundisha. Bwana wetu Yawe amenifanya kuwa musikilivu, nami sikukataa wala kurudia nyuma. Wale walionipiga, niliwaelekezea mugongo wangu, wale walioziongoa ndevu zangu, mashavu yangu. Sikuficha uso wangu wakati watu waliponitukana na kunitemea mate. Bwana wetu Yawe ananisaidia kwa hiyo siwezi kufazaika. Uso wangu nimeukaza kama jiwe; ninajua kwamba sitapata haya. Muteteaji wangu yuko karibu. Ni nani atakayepingana nami? Akuje tusambe naye. Adui yangu ni nani? Ajitokeze mbele basi. Angalia Bwana wetu Yawe ananisaidia. Ni nani anayeweza kusema niko na kosa? Waadui zangu wote watachakaa kama nguo, nondo watawatafuna. Nani kati yenu anayemwogopa Yawe? Nani anayetii maneno ya mutumishi wake? Kama kuna mutu anayetembea katika giza bila taa, amutumainie Yawe, na kumutegemea Mungu wake. Lakini ninyi munaowasha moto, na kujifanyia silaha za mienge, mutembee kwa mwangaza wa moto huo, ndimi za moto muliowasha ninyi wenyewe. Kitu mutakachopata kutoka kwa Yawe ni hiki: ninyi mutalala chini na mateso makali. Yawe anasema hivi: Munisikilize enyi munaotaka kukombolewa, ninyi munaonitafuta mimi Yawe. Muangalie jiwe mulilochongwa toka ndani yake, mulima mulimochimbuliwa. Mukumbuke Abrahamu babu yenu, na Sara aliyewazaa ninyi. Abrahamu alikuwa hana mutoto wakati nilipomwita, lakini nilimubariki na kumufanya kuwa na wengi. Mimi Yawe nitaufariji Sayuni, nitatengeneza pahali pake pote palipoharibika. Nitazifanya mbuga zake kama shamba la Edeni, jangwa yake kama bustani ya Yawe. Ndani yake kutapatikana furaha na shangwe, na nyimbo za shukrani zitasikilika humo. Munisikilize, enyi watu wangu, munitegee sikio, enyi taifa langu. Sheria na haki zitatoka kwangu mimi; nazo zitakuwa mwangaza wa mataifa. Ukombozi wangu unakaribia upesi; wokovu nitakaoleta unaanza kutokea. Mimi mwenyewe nitayatawala mataifa. Wakaaji wa inchi za mbali wananingojea, wanaitegemea nguvu yangu. Muinue macho, muangalie mbingu, kisha muangalie dunia kule chini. Mbingu zitatoweka kama moshi, dunia itachakaa kama nguo, na wakaaji wake watakufa kama vidudu. Lakini wokovu ninaouleta unadumu milele; ukombozi wangu hautakoma hata kidogo. Munisikilize, enyi munaojua mambo ya haki, ambao sheria zangu ziko ndani ya mioyo yenu. Musiogope mazarau ya watu, wala kufazaishwa na masimango yao. Maana watakuliwa na nondo kama vile nguo; vidudu watawakula kama wanavyokula nguo ya manyoya ya kondoo. Lakini ukombozi ninaouleta mimi utadumu milele; wokovu wangu hautakuwa na mwisho. Amuka! Amuka na nguvu, ee mukono wa Yawe! Amuka kama ulivyofanya hapo zamani, nyakati za vizazi vilivyopita. Si wewe ndiwe uliyemukatakata yule nyama mukubwa Rahabu, ukamutoboa yule nyoka mukubwa wa kuogopesha? Wewe ndiwe uliyekausha bahari, ndiwe uliyevikausha vilindi vya maji na kufanya njia katika vilindi vya bahari, kusudi wale uliowakomboa wavuke humo. Watu wako uliowakomboa, ee Yawe, watarudia, watakuja Sayuni wakiimba; watajaa furaha ya milele, watapata furaha na shangwe. Huzuni na maombolezo vitatoweka kabisa. Yawe anasema hivi: Mimi, kweli mimi, ndiye ninayekufariji. Kwa nini wewe unamwogopa mutu ambaye ni wa kufa, mwanadamu ambaye anatoweka kama majani? Wewe umenisahau mimi Yawe Muumba wako, niliyezitandaza mbingu, na kuiweka misingi ya dunia! Kwa sababu ya kasirani ya yule anayekutesa, unaendelea kuogopa siku zote kwamba yuko tayari kukuangamiza! Lakini hasira yake itafikia wapi? Wafungwa watafunguliwa upesi, hawatakufa na kushuka katika shimo, wala hawatakosewa chakula. Mimi ni Yawe, Mungu wako, ninayechafua bahari, zoruba yake ikinguruma; Yawe wa majeshi, ndilo jina langu! Nimeyaweka maneno yangu katika kinywa chako; nimekuficha katika kivuli cha mukono wangu. Mimi nilizitandaza mbingu, nikaiweka misingi ya dunia. Mimi ninawaambia, enyi watu wa Sayuni: Ninyi ni watu wangu. Amuka, ewe Yerusalema! Amuka usimame wima! Yawe amekukunywesha kikombe cha kasirani yake, nawe umekikunywa mpaka tone la mwisho, mpaka ukayumbayumba. Kati ya watoto wote uliowazaa hakuna yeyote wa kukuongoza. Hakuna hata mumoja wa kukushika mukono kati ya watoto wote uliowalea. Hasara hizi mbili zimekupata: uharibifu na maangamizi; njaa na mauaji. Nani atakayekuonea huruma? Nani atakayekufariji? Watoto wako wamezimia, wamelala pembeni ya kila barabara, wako kama paa aliyenaswa ndani ya mutego. Wamepatwa na kasirani ya Yawe, wamepatwa na azabu ya Mungu wako. Basi, sikiliza, ewe Yerusalema unayeteseka; sikiliza wewe uliyelewa, lakini sio kwa divai. Bwana, Yawe, Mungu wako, anayewatetea watu wake, anasema hivi: Nimekuondolea kikombe cha kuyumbisha, hautakunywa tena kikombe cha kasirani yangu. Nami nitakitia katika mikono ya wanaokutesa, waliokuambia ulalie tumbo wapite juu yako, nawe ukaufanya mugongo wako kama vile udongo wa njia, kama vile barabara ya kupitia. Amuka! Amuka! Ujipatie zile nguvu zako, ewe Sayuni! Uvae nguo yako nzuri, ewe Yerusalema, muji mutakatifu. Maana hawataingia tena kwako watu wasiotahiriwa na wachafu. Ujikungute mavumbi, usimame, ewe Yerusalema uliyekuwa mufungwa! Ujifungue minyororo yako katika shingo, ewe binti Sayuni uliyekamatwa mateka. Yawe anasema hivi: Ninyi muliuzishwa bure bila malipo yoyote, na mutakombolewa bila kulipa feza. Tena zamani ninyi watu wangu mulikimbilia Misri mukakaa kule. Halafu nyuma Waasuria waliwagandamiza bila sababu yoyote. Katika hali ya sasa ninapata faida gani kuwaona watu wangu wamepelekwa katika utumwa? –Ni ujumbe wa Yawe. Hao wanaowatawala wanajitapa. Nalo jina langu linaendelea kuzarauliwa kila siku. –Ni ujumbe wa Yawe. Kwa hiyo watu wangu watajua mimi ni nani. Siku hiyo watajua kwamba ni mimi ninayesema: “Niko!” Ni furaha kabisa! Mujumbe anatokea kwenye mulima. Anatangaza habari njema za amani, heri, na ukombozi. Anauambia Sayuni: Mungu wako anatawala! Sikiliza sauti ya walinzi wako; wanaimba pamoja kwa furaha, maana wanaona kwa macho yao wenyewe kurudi kwa Yawe katika Sayuni. Mupige kelele za shangwe, enyi mabomoko ya Yerusalema! Yawe amewafariji watu wake, ameukomboa Yerusalema. Yawe ameonyesha nguvu yake tukufu, mbele ya mataifa yote. Atawaokoa watu wake, na ulimwengu wote utashuhudia. Muondoke! Muondoke! Mutoke pale! Musiguse kitu chochote kichafu! Muondoke kule Babeli! Mujitakase, enyi munaobeba vyombo vya Yawe. Mara hii hamutatoka kwa haraka, wala hamutaondoka mbiombio! Maana Yawe atawatangulia, Mungu wa Israeli atawalinda nyuma yenu. Mungu anasema hivi: Mutumishi wangu atafanikiwa; atatukuzwa na kupewa cheo, atapata heshima kubwa. Wengi waliomwona walishituka, kwa vile sura yake ilikuwa imeharibika; hakukuwa tena na umbo la mwanadamu! Lakini sasa ameyashangaza mataifa mengi. Wafalme watapumbazika kwa sababu yake, maana wataona mambo ambayo hawajapata kuambiwa, na kufahamu mambo ambayo hawajapata kusikia. Ni nani aliyeamini mambo tuliyoyasikia? Mukono wa Mungu umefunuliwa kwa ajili ya nani? Maana, mbele ya Yawe, mutumishi wake alikomaa kama kichipukizi, kama muzizi katika inchi kavu. Hakukuwa na umbo wala sura ya kupendeza, wala hakukuwa na uzuri wowote wa kutuvuta. Alizarauliwa na kukataliwa na watu. Alikuwa mutu wa uchungu na huzuni. Alikuwa kama mutu wa kuchukiza kwa watu; alizarauliwa na tukamwona si kitu. Hata hivyo alitwaa mateso yetu, na kubeba huzuni zetu. Sisi tulifikiri amepata azabu, amepigwa na Mungu na kuteswa. Lakini aliumizwa kwa sababu ya zambi zetu, alipondwa kwa sababu ya maovu yetu. Kwa kuazibiwa kwake sisi tumepata uzima; kwa kupigwa kwake sisi tumepona. Sisi wote tumepotea kama kondoo, kila mumoja wetu ameelekea njia yake. Lakini Yawe alimubebesha azabu, ambayo sisi wenyewe tuliistahili. Alionewa na kuteswa, lakini alivumilia kwa unyenyekevu, bila kutoa sauti hata kidogo. Alikuwa kama mwana-kondoo anayepelekwa kwenda kuchinjwa, kama kondoo anavyokaa kimya anapokatwa manyoya. Hakutoa sauti hata kidogo. Alikamatwa kwa kinguvu, akahukumiwa na kupelekwa kuuawa; na hakuna mutu aliyejali mambo yanayomupata. Alifukuzwa kutoka inchi ya wanaokuwa wazima, kwa sababu ya makosa ya watu wangu. Walimuzika pamoja na waovu; katika kifo aliwekwa pamoja na watajiri, ingawa hakutesa watu hata kidogo, wala hakusema neno lolote la udanganyifu. Yawe alipenda kumuponda kwa mateso. Alitoa uzima wake kwa ajili ya kuondoa zambi. Mutumishi wa Mungu atakuwa na wazao; ataishi maisha marefu. Yeye ndiye atakayetimiza mupango wa Yawe. Mungu anasema: Kisha kutaabika sana, mutumishi wangu atafurahi. Kwa njia ya kujulikana kwa huyo mutumishi wangu wa haki, atawafanya wengi wakuwe wenye haki, naye atazibeba zambi zao. Kwa hiyo nitamugawanyia sehemu pamoja na wakubwa, atagawanya vitu vilivyotekwa pamoja na wenye nguvu. Alijitoa yeye mwenyewe hata kufa; aliwekwa kundi moja na watu wakosaji. Alizibeba zambi za watu wengi, akawaombea musamaha hao wakosaji. Yawe anasema hivi: Imba kwa shangwe, ewe unayekuwa tasa, wewe ambaye haujapata kuzaa! Piga kelele na kuimba kwa nguvu, wewe usiyepata kuzaa mutoto. Maana watoto wako wewe uliyeachwa watakuwa wengi kuliko wa yule anayekuwa na mume. Panua nafasi katika hema yako, ongeza mapazia ya makao yako, usijali mali unayotumia. Urefushe kamba zako, na kuimarisha misumari yako; maana utapanuka kila upande; wazao wako watarizi mataifa, miji iliyokuwa ukiwa itajaa watu. Usiogope, hautapata haya tena. Usifazaike, hautazarauliwa tena. Utaisahau haya uliyopata katika ujana wako, wala hautakumbuka tena mazarau ya ujane wako. Muumba wako atakuwa mume wako. Jina lake Yawe wa majeshi. Mukombozi wako ni Mutakatifu wa Israeli. Yeye anaitwa Mungu wa Ulimwengu Wote. Yerusalema, Yawe amekuita tena. Ulikuwa kama vile muke aliyeachwa na kuhuzunika. Mungu wako anasema: Muke aliyeolewa akiwa kijana, anaweza kuachiliwa? Nilikuacha kwa muda mufupi tu. Kwa huruma nyingi, nitakurudisha. Kwa hasira nyingi nilikuficha uso wangu kwa muda kidogo, lakini kwa wema wa milele nitakuonea huruma. Ni Yawe Mukombozi wako anayesema hivyo. Nitafanya kama nilivyofanya wakati wa Noa. Wakati ule niliapa kwamba sitaifunika tena dunia kwa mafuriko ya maji. Basi sasa ninaapa kwamba sitakukasirikia tena wala sitakukaripia tena. Milima inaweza kutoweka, vilima vinaweza kuondolewa, lakini rehema zangu kwako sitaziacha, agano langu la amani litaimarishwa. Ni Yawe anayekuhurumia anayesema hivyo. Ewe Yerusalema, uliteseka, ulitaabishwa na kukosa wa kukufariji, lakini nitakujenga upya kwa mawe ya bei kali, misingi yako itakuwa ya mawe ya yakuti. Minara yako nitaijenga kwa mawe ya akiki, milango yako kwa almasi, na ukuta wako kwa mawe ya bei kali. Watu wako watafundishwa nami Yawe, wana wako watapata ustawi mwingi. Utaimarishwa katika haki, mbali na kaoneo, nawe hautaogopa kitu; mbali na hofu, maana haitakukaribia. Mutu yeyote akikuja kukushambulia, hatakuwa ametumwa nami. Yeyote atakayekushambulia, ataangamia mbele yako. Mimi ndiye niliyemwumba mufuaji wa vyuma, anayewasha moto wa makaa na kufua silaha. Ni mimi vilevile niliyemwumba mwangamizaji anayeangamiza. Silaha zote zilizotengenezwa kwa kukuzuru wewe hazitafaa kwa kitu chochote. Mutu akikushitaki, utamushinda. Hiyo ndiyo haki niliyowapangia watumishi wangu. Hizo ndizo haki nilizowahakikishia. –Ni ujumbe wa Yawe. Ee ninyi wote wenye kiu mukuje kwenye maji! Mukuje, wote hata musiokuwa na feza; mununue chakula na mupate kula, mununue divai na maziwa. Bila feza, bila malipo! Mbona munatumia feza zenu kwa ajili ya kitu kisichokuwa chakula? Kwa nini kutoa jasho lenu kwa kitu kisichoshibisha? Munisikilize mimi kwa uangalifu, nanyi mutakula vinavyokuwa vitamu, na kufurahia vinavyokuwa bora. Mutege sikio, enyi watu wangu, mukuje kwangu; munisikilize, kusudi mupate kuishi. Nami nitafanya nanyi agano la milele; nitawatendea mema niliyomwahidi Daudi. Mimi nilimufanya kuwa mukubwa na mutawala wa mataifa kusudi yeye anishuhudie kwa watu wa mataifa. Sasa utayaita mataifa usiyoyajua, watu wa mataifa yasiyokutambua watakuja mbio kwenu, kwa sababu yangu mimi Yawe, Mungu wako; kwa sababu yangu mimi Mutakatifu wa Israeli niliyekufanya wewe upate utukufu. Mumutafute Yawe wakati angali anaweza kupatikana, mumwombe musaada wakati angali karibu. Waovu waache njia zao mbaya, watu wabaya waachane na mawazo yao mabaya; wamurudilie Yawe apate kuwahurumia, wamwendee Mungu wetu maana atawasamehe. Maana mawazo yangu si kama mawazo yenu, wala njia zangu si kama njia zenu. –Ni ujumbe wa Yawe.– Kama vile mbingu zinavyokuwa mbali na dunia, ndivyo njia zangu zinavyokuwa mbali na zenu, na mawazo yangu mbali na mawazo yenu. Kama vile mvua na teluji inavyoshuka toka mbinguni, wala hairudi kule lakini inalowanisha udongo, kuuzalisha na kuchipukiza mimea, na kumupatia mupandaji mbegu na kuwapa watu chakula, ni vilevile na neno langu mimi: halitanirudilia bila mafanikio, lakini litatimiza mapenzi yangu, litafikia shabaha nililoliwekea. Mutatoka Babeli kwa furaha; mutaongozwa muende kwa amani. Milima na vilima mbele yenu vitapiga kelele na kuimba, na miti yote katika mashamba itawapigia mikono. Pahali pa miiba kutaota miti ya shindano, na pahali pa michongoma kutaota misunobari. Hilo litakuwa jambo litakalowakumbusha watu juu ya mambo niliyotenda mimi Yawe, kitambulisho cha milele ambacho hakitafutwa. Yawe anasema hivi: Mufuate sheria yangu na kutenda kwa haki, maana ninakaribia kuwaokoa, watu wataona wazi kwamba ninawakomboa. Heri mutu anayefuata maneno hayo, anayeshika kabisa siku za Sabato kwa heshima na kuepuka kutenda uovu wowote. Mugeni anayenitambua mimi Yawe asifikiri hivi: Hakika Yawe atanitenga na watu wake. Naye towashi asiseme: Mimi ni muti wenye kukauka! Maana Yawe anasema hivi: Towashi anayeshika siku zangu za Sabato, anayefanya mambo yanayonipendeza, na kuchunga agano langu, nitamupatia nafasi ya ukumbusho na ya sifa katika nyumba yangu na kuta zangu, nafasi bora kuliko kuwa na wana na wabinti. Nitamupatia jina la kukumbukwa siku zote na ambalo halitafutwa hata kidogo. Wageni watakaoshikamana nami Yawe, kwa kunitumikia na kwa kupenda jina langu, na kuwa watumishi wangu, wote watakaoshika siku ya Sabato bila kuichafua, watu watakaofuata agano langu, hao nitawaleta katika mulima wangu mutakatifu, na kuwafurahisha katika nyumba yangu ya maombi; sadaka zao na sadaka za kuteketezwa zitakubaliwa kwenye mazabahu yangu. Maana nyumba yangu itaitwa: Nyumba ya maombi kwa ajili ya watu wote. –Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe, yule anayewakusanya Waisraeli waliosambazwa.– Zaidi ya hao niliokwisha kukusanya, nitawakusanya watu wengine wakutane nao. Enyi nyama wote wakali, nanyi nyama wote wa pori, mukuje mukule. Maana walinzi wa Israeli wote ni vipofu; wote hawana akili yoyote. Wote ni kama imbwa bubu wasioweza kufoka, wanalala tu na kuota ndoto, wanapenda sana kusinzia! Hao ni kama imbwa walafi sana, wala hawawezi kutosheka hata kidogo. Wachungaji nao hawana akili yoyote. Kila mumoja anatafuta njia yake mwenyewe, kila mumoja anatafuta faida yake. Wao wanaambiana hivi: Mukuje, tuende kutafuta divai; mukuje tukunywe tushibe kinywaji kikali! Kesho itakuwa kama leo, tena itakuwa sikukuu kubwa zaidi. Mutu wa haki akikufa, hakuna mutu anayejali; mutu mwema akihamishwa toka dunia, hakuna mutu anayefikiri na kusema: Mutu huyo mwema amehamishwa kusudi asipatwe na hasara, kusudi apate kuingia kwenye amani. Watu wenye mwenendo sawa, watakuwa na amani na kupumzika. Lakini Yawe anasema: Mukuje hapa ninyi wana wa wake wachawi; ninyi wazao wa wachawi, wazinzi na makahaba. Ni nani munayemuchekelea? Munamuzomea nani na kumutoshea ulimi inje? Ninyi wenyewe ni waasi tangu mwanzo, ninyi ni kizazi kidanganyifu. Ninyi munawaka tamaa kwenye miti ya mialo, na chini ya kila muti wenye kuwa na majani mabichi. Munawachinja watoto wenu na kuwatambikia katika mabonde na ndani ya nyufa za mawe. Munachagua mawe laini katika mabonde, na kuyafanya kuwa mungu wenu. Munayamwangia sadaka ya kinywaji na kuyapelekea sadaka ya unga! Mimi nitatulizwa kwa vitu hivyo? Mumeweka vitanda vyenu juu ya milima mirefu, na kwenda kule kwa kutambikia. Nyuma ya milango na miimo mumetundika sanamu yenu. Ninyi munaniacha mimi. Mumevua nguo zenu na kupanda juu ya vitanda vyenu vipana. Mumelipa wapenzi wenu ambao munataka kulala nao. Halafu munatimiza tamaa zenu mbaya. Munajipakaa marasi na mafuta kwa wingi kisha munakwenda kumwabudu Moleki. Munawatuma wajumbe wenu huko na huko, kujitafutia miungu ya kuabudu; hata kuzimu walifika. Mulichoka na safari zenu ndefu, hata hivyo hamukukata tamaa; mulijipatia nguvu mupya, ndiyo maana hamukuzimia. Mulimwogopa na kutishwa na nani hata mukasema uongo, mukaacha kunikumbuka mimi na kuacha kabisa kufikiri juu yangu? Mimi sikuwaambia kitu kwa muda murefu; ndiyo maana labda mukaacha kuniheshimu! Munafikiri kwamba munafanya sawa, lakini nitayafichua matendo yenu, nayo miungu yenu haitawafalia kitu. Mutakapolia kwa kuomba musaada, basi ile lundo ya sanamu zenu iwaokoe! Upepo utavipeperushia mbali; pumzi itavitupilia mbali. Lakini watakaotafuta kimbilio kwangu, watarizi inchi, mulima wangu mutakatifu utakuwa mali yao. Yawe anasema hivi: Mujenge! Mujenge! Mutayarishe njia! Muondoe vikwazo vyote katika njia ya watu wangu! Hivi ndivyo anavyosema Mungu anayekuwa juu kabisa, anayeishi milele na ambaye jina lake ni Mutakatifu: Mimi ninakaa kule juu, Pahali Patakatifu, ninakaa vilevile na wenye majuto na wanyenyekevu. Mimi nitawatia moyo wanaokuwa wanyenyekevu na kuwapa nguvu wenye majuto. Maana sitaendelea kugombana wala kuwakasirikia siku zote, maana hao niliowaumba watazimia mbele yangu, nami ndiye niliyewapa pumzi yangu ya uzima. Niliwakasirikia kwa sababu ya uovu na tamaa zao; niliwaazibu, nikauficha uso wangu na kukasirika. Lakini wao waliendelea kufuata njia zao wenyewe. Niliona mwenendo wao, lakini nitawaponyesha; nitawaongoza na kuwapa faraja, nitawatuliza hao wanaoomboleza. Mimi nitawapa amani, amani kwa wanaokuwa mbali na wanaokuwa karibu! –Ni Yawe anayesema hivyo.– Mimi nitawaponyesha. Lakini waovu ni kama bahari iliyochafuka, ambayo haiwezi kutulia; maji yake yanatupa matope na takataka. Mungu wangu anasema hivi: Hakuna amani kwa watu waovu. Yawe anasema: Piga kelele, wala usijizuize; ulalamike kwa sauti kubwa kama baragumu. Uwatangazie watu wangu makosa yao, uwaambie wazao wa Yakobo zambi zao. Kila siku wananitafuta, wanatamani kujua njia zangu, kama vile wao ni taifa linalotenda haki, taifa lisilosahau agizo la Mungu wao. Wanataka niamue kwa haki, na kutamani kuikaa karibu na Mungu. Ninyi munaniuliza: Kwa nini tunafunga kula lakini wewe hauoni? Mbona tunajitesa, lakini wewe haujali? Ukweli ni kwamba wakati munapofunga kula, munatafuta tu furaha yenu wenyewe na kuwagandamiza watumishi wenu! Munafunga kula lakini munagombana na kupigana mangumi vikali. Mukifunga namna hiyo, maombi yenu hayatafika kwangu juu. Munapofunga kula, ninyi munajitaabisha; munaviinamisha vichwa vyenu kama utete, na kulalia nguo za magunia na majivu. Hii ndio munayoita mafungo ya kula chakula? Hiyo ni siku inayonipendeza mimi? Mafungo ninayotaka mimi ni haya: kuwafungua waliofungwa bila haki, kuziondoa kamba za utumwa, kuwaacha huru wanaogandamizwa, na kuvunja kabisa mambo yote ya kitumwa! Mafungo ya kweli ni kugawanya chakula chako pamoja na wenye njaa, kuwakaribisha katika nyumba yako wamasikini wasiokuwa na makao, kuwavalisha wasiokuwa na nguo, bila kusahau kuwasaidia wandugu zenu. Mukifanya hivyo mutaonekana kama mwangaza wa mapambazuko, na mutapona haraka. Matendo yenu mema yatawatangulia, nami nitawalinda kutoka nyuma kwa utukufu wangu. Halafu mutaomba, nami Yawe nitawaitikia; mutalia kwa sauti kwa kuomba musaada, nami nitajibu hivi: Niko hapa! Kama mukiondoa mambo ya kitumwa, mukiacha kuzarau wengine na kusema maovu, mukiwapa wenye njaa chakula, mukitimiza mahitaji ya wenye kuteswa, mwangaza utawaangazia nyakati za giza, giza lenu litakuwa kama muchana. Mimi Yawe nitawaongoza siku zote, nitatimiza mahitaji yenu wakati wa shida. Nitawaimarisha katika mwili, nanyi mutakuwa kama bustani iliyomwangiliwa maji, kama chemichemi ya maji ambayo maji yake hayakauki hata kidogo. Watu wako watajenga tena mabomoko ya zamani; mutajenga upya juu ya misingi iliyoachwa zamani. Nanyi mutaitwa watu waliotengeneza upya kuta, watu waliotengeneza tena barabara za miji. Kama ukiacha kufanya kazi siku ya Sabato, ukiacha shuguli zako siku yangu hiyo takatifu, ukiifanya siku yangu kuwa ya furaha, ukiheshimu siku hiyo takatifu ya Yawe, ukiacha shuguli zako au kupiga domo, utapata furaha yako kwangu mimi Yawe, nitakupatia ushindi katika kila upinzani katika inchi, nitakulisha mali ya Yakobo, babu yako. Maneno haya yanatoka katika kinywa cha Yawe. Musifikiri kwamba mukono wa Mungu ni mufupi, hata asiweze kuwaokoa, au kwamba masikio yake yamefungana, hata asiweze kuwasikiliza ninyi. Zambi zenu ndizo zinazowatenga na Mungu wenu, zambi zenu zimemufanya ajifiche mbali nanyi hata asiweze kuwasikiliza ninyi. Maana mikono yenu imechafuka kwa damu, na vidole vyenu kwa matendo maovu. Midomo yenu imesema uongo, na ndimi zenu zinasema uovu. Hakuna anayemushitaki mwenzake kwa haki, wala anayejitetea kwa ukweli. Munategemea mambo ya bure; munasema uongo. Munafanya mipango ya kuleta hasara na kuzaa uovu. Munatoa mayai ya nyoka yenye sumu, munafuma wavu wa buibui. Anayekula mayai yenu anakufa, na yakipasuliwa, nyoka anatokea ndani yake. Wavu wenu haufai kama nguo, watu hawawezi kujifunikia munachofuma. Kazi zenu ni kazi za uovu, matendo yenu yote ni mateso makali. Muko mbio kutenda maovu, muko wepesi kumwanga damu isiyokuwa na kosa. Mawazo yenu ni mawazo ya uovu, popote munapokwenda munaacha ukiwa na uharibifu. Njia ya amani hamuijui hata kidogo; hamufuati sheria ya Mungu. Mumejifanyia njia potovu, yeyote anayepitia humo hapati amani. Kwa hiyo, kufuata sheria ya Mungu kuko mbali nasi, haki haifiki kwetu. Tulitazamia kupata mwangaza, kumbe ni giza tupu; tulingojea mwangaza, lakini tunatembea katika giza. Kama vipofu tunapapasapapasa ukuta; tunasitasita kama watu wasiokuwa na macho. Tunajikwaa muchana kati, sawa vile ni usiku; kati ya wenye afya, sisi ni kama wafu. Tunanguruma kama dubu, tunaomboleza kama njiwa. Tunatazamia watu wanaofuata sheria ya Mungu, lakini hakuna, tunatazamia wokovu, lakini uko mbali nasi. Makosa yetu mbele yako ni mengi sana, zambi zetu zinashuhudia juu yetu. Kweli, makosa yetu yanaandamana nasi, tunayajua maovu yetu. Tumekuasi na kukukana, ee Yawe, tumekataa kukufuata, ewe Mungu wetu. Tunasema maneno ya kutesa na uasi, katika mioyo yetu tunatunga na kutoa maneno ya uongo. Sheria ya Mungu imewekwa pembeni, haki iko mbali; ukweli unakanyagwa katika tribinali, usawa hauwezi kuingia humo. Ukweli umekosekana, naye anayeacha uovu ananyanganywa. Mungu aliona mambo hayo. Alichukizwa kwamba watu hawafuati sheria yake. Aliona kwamba hakuna mutu aliyejali, akashangaa kwamba hakuna aliyeingilia kati. Basi akaamua kunyoosha mukono wake mwenyewe, haki yake ikamusaidia. Alivaa haki kama vile nguo ya kujikinga kifua, na wokovu kama kofia ya chuma juu ya kichwa. Alivaa nguo ya kulipiza kisasi, na kujifunika na kanzu ya wivu. Atawaazibu waadui kadiri ya matendo yao, kasirani yake na kisasi vitawapata waadui zake; atawaazibu hata wakaaji wa inchi za mbali. Toka magaribi mpaka mashariki, kila mutu atamwogopa Yawe na kutambua utukufu wake. Maana atakuja kama muto wenye kuporomoka mbio, muto unaosukumwa kwa upepo wa Yawe. Naye atakuja katika Sayuni kama Mukombozi, Mukombozi wa wazao wa Yakobo ambao wataachana na makosa yao. –Ni ujumbe wa Yawe. Yawe anasema: Mimi ninafanya nanyi agano hili: Roho wangu anayekuwa juu yenu, maneno niliyoyaweka katika kinywa chenu, hayataondoka kwenu hata kidogo, wala kwa watoto na wajukuu wenu, tangu sasa na hata milele. Simama, ee Sayuni uangaze; maana mwangaza unatokea kwa ajili yako, utukufu wa Yawe unakuangazia. Giza litaifunika dunia, giza kubwa litayafunika mataifa; lakini wewe, Yawe atakuangazia, utukufu wake utaonekana kwako. Mataifa watatembea katika mwangaza wako, wafalme watavutwa na kungaa kwako. Inua macho uangalie pande zote; wote wanakusanyika wakuje kwako. Wana wako watafika toka mbali, wabinti zako watabebwa katika mikono. Halafu utaona na utafurahi, moyo wako utasisimuka na kushangilia. Maana utajiri tokea ngambo ya bahari utakufikia kwa wingi, mali za mataifa zitaletwa kwako. Makundi ya ngamia yataifunika inchi yako, wana wa ngamia kutoka Midiani na Efa; wote watakuja kutoka Seba. Watakuletea zahabu na ubani, wakitangaza sifa za Yawe. Makundi ya nyama wa inchi ya Kedari yatakusanyika kwako, utaweza kuwatumia kondoo dume wa Nebayoti; utatoa sadaka inayokubaliwa kwenye mazabahu ya Mungu, naye ataitukuza nyumba yake tukufu. Nani hao wanaopita mbio kama mawingu, kama njiwa wanaoruka kwenda katika chicha zao? Ni mashua zinazotoka katika inchi za mbali, zikitanguliwa na mashua za Tarsisi. Zinawaleta watoto wako, pamoja na feza na zahabu yao, kwa sifa ya Yawe, Mungu wako, kwa sifa ya Mungu, Mutukufu wa Israeli, maana amewafanya mupate utukufu. Yawe anasema: Wageni watazijenga upya kuta zako, wafalme wao watakutumikia. Maana kwa hasira yangu nilikupiga, lakini kwa wema wangu nimekuhurumia. Milango yako itakuwa wazi siku zote; usiku na muchana haitafungwa, kusudi watu wakuletee utajiri wa mataifa, pamoja na wafalme wao katika maandamano. Kila ufalme au taifa lisilokutumikia litaangamizwa; mataifa hayo yatateketezwa kabisa. Utaletewa utukufu wa pori ya Lebanoni: mbao za shindano, mivinje na misunobari, zitumike kwa kupamba kiwanja cha hekalu langu; nami nitaleta utukufu hapo ninapokaa. Wazao wa wale waliokutesa, watakuja na kuinama uso mpaka chini mbele yako. Wote wale waliokuzarau, watapiga magoti kwenye miguu yako. Watakuita: “Muji wa Yawe”, “Sayuni”, “Muji wa Mutakatifu wa Israeli”. Wewe ulikuwa umeachwa na kuchukiwa, hakuna aliyependa hata kupita ndani yako. Lakini sasa nitakufanya ukuwe na utukufu milele, utakuwa muji wa furaha kwa kizazi na kizazi. Utaletewa chakula na watu wa mataifa; wafalme watakupatia chakula bora. Hapo utatambua kwamba mimi Yawe ni Mwokozi wako; mimi Mwenye Nguvu wa Yakobo ni Mukombozi wako. Pahali pa shaba nitakuletea zahabu, pahali pa chuma nitakuletea feza, pahali pa miti, nitakuletea shaba, na pahali pa mawe nitakuletea chuma. Amani itatawala juu yako, haki itakuongoza. Mateso makali hayatasikilika tena katika inchi yako; wala uharibifu na maangamizi ndani ya mipaka yako. Utaweza kuziita kuta zako: “Wokovu”, na milango yako: “Sifa”. Hautahitaji tena jua kukuangazia muchana, wala mwezi kukuangazia usiku; maana mimi Yawe ni mwangaza wako milele; mimi Mungu wako nitakuwa utukufu wako. Mwangaza wako muchana hautatua kama jua, wala mwangaza wako usiku kufifia kama mbalamwezi; maana Yawe ni mwangaza wako milele, nazo siku zako za kuomboleza zitakoma. Watu wako wote watakuwa wa haki, nao watarizi inchi milele. Hao ni chipukizi nililopanda mimi, kazi ya mikono yangu kwa ajili ya utukufu wangu. Anayekuwa jamaa ndogo kati yenu atakuwa kabila, anayekuwa mudogo kuliko wote atakuwa taifa kubwa. Mimi ndiye Yawe; wakati utakapofika nitayatimiza haraka. Roho wa Bwana wetu Yawe yuko pamoja nami, maana Yawe amenichagua, akanituma niwahubirie wanaoteswa habari njema, niwatunze waliovunjika moyo, niwatangazie waliohamishwa kwamba watapata uhuru, na wafungwa kwamba watafunguliwa. Amenituma kutangaza mwaka wake wa neema, na siku ya Mungu wetu ya kulipiza kisasi kusudi niwafariji wote wanaoomboleza. na kuwapa wale wanaoomboleza katika Sayuni taji la maua pahali pa majivu juu ya kichwa, mafuta ya kuangarisha kwa furaha pahali pa maombolezo, nguo ya sifa pahali pa moyo muzito. Nao wataitwa miti ya mialo ya haki, Yawe aliyopanda kuonyesha utukufu wake. Watayajenga upya mabomoko ya zamani, wataisimika miji iliyoharibika tangu mbele; wataitengeneza miji iliyobomolewa, uharibifu wa vizazi vingi vilivyopita. Wageni watakuwa hapo kuwachungia makundi yenu ya nyama; watawalimia na kuwatunzia mizabibu yenu. Nanyi mutaitwa: “Makuhani wa Yawe”, Mutaitwa: “Watumishi wa Mungu wetu”. Mutafaidika kwa utajiri wa mataifa, mutatukuzwa kwa mali zao. Kwa vile mulipata haya mara mbili, watu wakaona kwamba mazarau ni majaliwa yenu, sasa mutapata sehemu mara mbili kuwa mali yenu, na furaha yenu itadumu milele. Mimi Yawe ninapenda watu wafuate sheria yangu; ninachukia unyanganyi na uovu. Nitawatunza watu wangu kwa uaminifu, nitafanya nao agano la milele. Wazao wao watajulikana kati ya mataifa; watajulikana kati ya watu wengine. Kila mutu atakayewaona atakubali kwamba wao ni watu waliobarikiwa na Yawe. Nitafurahi sana kwa sababu ya Yawe, nafsi yangu itashangilia kwa sababu ya Mungu wangu. Maana amenivalisha nguo ya wokovu, amenifunika kanzu ya haki, kama bwana arusi anavyojipamba kwa shada la maua, kama bibi arusi anavyojipamba kwa ushanga wake. Hivyo, kama vile udongo unavyootesha mimea, na shamba linavyochipukiza mbegu zilizopandwa humo, Yawe atasababisha haki na sifa kuonekana mbele ya mataifa yote. Kwa ajili ya Sayuni sitakaa kimya, kwa ajili ya Yerusalema sitatulia, mpaka kuokolewa kwake kuonekane kama umeme, wokovu wake utokee kama mwangaza. Mataifa watauona wokovu wako, wafalme wote watauona utukufu wako. Nawe utaitwa kwa jina jipya ambalo litapangwa na Yawe mwenyewe. Utakuwa taji zuri katika mukono wa Yawe; taji la kifalme katika mukono wa Mungu wako. Hautaitwa tena: Aliyeachwa, wala inchi yako haitaitwa: “Ukiwa”. Lakini utaitwa: “Ninamufurahia”, na inchi yako itaitwa: “Aliyeolewa”. Maana Yawe amependezwa nawe, naye atakuwa kama mume wa inchi yako. Maana kama vile kijana mwanaume anavyomwoa binti, ndivyo aliyekujenga atakavyokuwa mume wako. Kama bwana arusi anavyofurahi juu ya bibi arusi, ndivyo Mungu atakavyofurahi juu yako. Juu ya kuta zako, ee Yerusalema, nimeweka walinzi, usiku na muchana hawatakaa kimya hata kidogo. Enyi munaomukumbusha Yawe ahadi yake, musikae kimya; musimupe hata nafasi ya kupumzika, mpaka atakapousimika Yerusalema, na kuufanya kuwa wenye sifa katika ulimwengu wote. Yawe ameapa kwa uwezo wake mukubwa, ameapa kwa nguvu yake akisema: Sitawapa tena waadui zako ngano yako; wala wageni hawatakunywa tena divai yako ambayo umeitoshea jasho. Lakini ninyi muliovuna ngano hiyo, mutaikula na kunitukuza mimi Yawe. Ninyi muliochuma mizabibu hiyo, mutakunywa divai yake katika viwanja vya hekalu langu takatifu. Enyi wakaaji wa Yerusalema, mutoke, mutoke inje ya muji, muwatayarishie njia watu wenu wanaorudia! Mujenge! Mujenge barabara na kuondoa mawe yote! Muweke bendera kuwa kitambulisho kwa ajili ya watu. Yawe ametangaza katika dunia yote, muwaambie watu wa Sayuni hivi: Mukombozi wenu anakuja, yeye anakuja na mapato yake, anafika na mushahara wake. Ninyi mutaitwa: Watu Watakatifu, Watu waliokombolewa na Yawe. Nawe Yerusalema utaitwa: Muji Mungu anaoupenda, Muji ambao Mungu hakuuacha. Ni nani huyu anayekuja kutoka Edomu, anayefika kutoka Bosira na nguo ya madoa mekundu? Ni nani huyo aliyevaa nguo ya utukufu, anatembea kwa nguvu zake kubwa? Ni mimi Yawe ninayetangaza ushindi wangu; nami ni mwenye nguvu ya kuokoa. Lakini mbona nguo yako ni nyekundu, nyekundu kama ya mutu anayekamua mizabibu? Kweli, nimekamua mizabibu peke yangu, wala hakuna mutu aliyekuja kunisaidia. Nimeyakanyaga mataifa kwa hasira yangu, niliyapondaponda kwa kasirani yangu. Nguo zangu zimejaa madoa ya damu yao, imechafua kabisa nguo yangu. Niliamua kwamba siku ya kulipiza kisasi imefika; wakati wa kuwakomboa watu wangu umefika. Niliangalia, hapakukuwa wa kunisaidia; nilishangaa, hapakukuwa wa kuniunga mukono. Lakini nilijipatia ushindi kwa mukono wangu, kasirani yangu ilinisaidia. Kwa hasira yangu niliwaponda watu, niliwalewesha kwa kasirani yangu; damu yao niliimwanga chini. Nitakumbusha mema ya Yawe, sifa za Yawe, matendo yake yote kwetu, mambo mazuri aliyowatendea Waisraeli, rehema yake, na wingi wa wema wake. Maana alisema juu yao: Hakika, hawa ni watu wangu; watoto wangu ambao hawatanidanganya. Basi yeye akakuwa Mwokozi wao. Katika taabu zao zote, hakumutuma mujumbe mwingine kwa kuwasaidia, lakini yeye mwenyewe alikuja kuwaokoa; kwa upendo na huruma yake aliwakomboa. Aliwabeba na kuwakamata tangu zamani. Lakini wao waliasi, wakaihuzunisha roho yake takatifu. Basi, Mungu akageuka, akakuwa adui yao; yeye mwenyewe akapigana nao. Halafu walikumbuka siku za zamani, wakati wa Musa, mutumishi wa Yawe. Wakauliza: Yuko wapi sasa Yawe, aliyewaokoa wachungaji wa kundi lake katika bahari? Yuko wapi yule aliyeweka Roho wake Mutakatifu kati yao, ambaye kwa mukono wake wenye nguvu alifanya maajabu kwa njia ya Musa, akapasua bahari na kuwaongoza watu wake, na kujipatia jina la milele? Aliwaongoza katikati ya vilindi vya bahari, wakapita humo kama farasi bila kujikwaa. Kama vile ngombe wanavyopelekwa kwa kulishwa katika bonde, ndivyo Roho wa Mungu alivyowapumzisha watu wake. Ndivyo, ee Mungu ulivyowaongoza watu wako, nawe ukajipatia jina tukufu. Utuchungulie kutoka mbinguni, ee Mungu, uone, utuangalie kutoka makao yako matakatifu na matukufu. Iko wapi bidii yako kwa ajili yetu na nguvu yako? Hatuoni tena upendo na huruma yako. Maana wewe ndiwe Baba yetu; Abrahamu, babu yetu, hatujali, naye Israeli hatutambui; lakini wewe, ee Yawe, ni Baba yetu. Wewe umeitwa tangu zamani: Mukombozi wetu. Ee Yawe, mbona unatukosesha njia zako? Mbona unaifanya mioyo yetu kuwa migumu hata tusikuogope? Urudie, ee Mungu, kwa ajili ya watumishi wako, makabila ambayo yalikuwa mali yako siku zote. Sisi watakatifu wako tulirizi inchi kwa muda kidogo tu, lakini waadui zetu wakakuja wakaharibu hekalu lako. Tumekuwa kama watu ambao haujawatawala hata kidogo, kama watu ambao hawakujulikana kwa jina lako. Heri ungepasua mbingu ushuke chini, milima ingetetemeka mbele yako! Ingeteketea kama moto unavyochoma kichaka, kama vile moto unavyochemusha maji. Ukuje upate kuwajulisha waadui zako jina lako nayo mataifa yatetemeke mbele yako! Wakati ulipotenda maajabu ambayo hatukutazamia, ulishuka chini nayo milima ikatetemeka ilipokuona. Tangu zamani hakuna aliyepata kusikia kwa masikio yake wala kumwona Mungu anayekuwa kama wewe, anayetenda mambo kama hayo kwa ajili ya wale wanaomutegemea! Wewe unakuja kuwasaidia wanaotenda haki kwa furaha, wanaokukumbuka na kufuata njia zako. Ulitukasirikia tulipokuwa wenye zambi; sisi tumeasi kwa muda murefu. Sisi wote tumekuwa kama watu wachafu; matendo yetu yote mema ni kama nguo chafu. Wote tunanyauka kama majani, uovu wetu unatupeperusha kama upepo. Hakuna hata mumoja anayekuja kukuomba; hakuna anayejishugulisha kukutafuta. Wewe unauficha uso wako mbali nasi, umetuacha tufungwe na maovu yetu. Hata hivyo, ee Yawe, wewe ni Baba yetu. Sisi ni kama udongo, wewe ni mufinyanzi. Sisi wote ni kazi ya mikono yako. Usitukasirikie sana, ee Yawe, usiukumbuke uovu wetu siku zote! Ukumbuke kwamba sisi wote ni watu wako! Miji yako mitakatifu imekuwa jangwa; Sayuni umekuwa matongo, Yerusalema umekuwa uharibifu. Nyumba yetu takatifu na nzuri, ambamo babu zetu walikusifu, imeteketezwa kwa moto. Pahali petu pote pazuri pamekuwa mabomoko. Mbele ya hayo yote utajizuiza usifanye kitu? Utaendelea kunyamaza tu, ee Yawe, na kututesa kupita kipimo? Yawe anasema; Nilikuwa tayari kujionyesha kwao wasiouliza habari zangu. Nilikuwa tayari kuwapokea wale wasionitafuta. Nililiambia taifa ambalo halikuomba kwa jina langu: Niko hapa! Niko hapa! Muchana kutwa niliwanyooshea mikono watu waasi, watu ambao wanafuata njia zisizokuwa nzuri, watu ambao wanafuata mawazo yao wenyewe. Ni watu ambao wananichokoza waziwazi siku zote; wanatambikia miungu yao katika bustani, na kuifukizia ubani juu ya matofali. Wanaikaa katika makaburi na kupitisha usiku ndani ya mashimo. Wanakula nyama ya nguruwe na kuweka muchuzi wa nyama wachafu ndani ya sahani zao. Wanawaambia wale wanaokutana nao hivi: Muikae mbali nami; musinikaribie kwa sababu mimi ni mutakatifu! Watu hao wananikasirikisha sana, hasira yangu ni kama moto usiozimika. Mujue kwamba mambo hayo yameandikwa mbele yangu, sitanyamaza lakini nitawalipiza; nitawalipa sawa inavyostahili. Nitawalipiza maovu yao wayalipe vilevile maovu ya babu zao. –Ni Yawe anayesema hivyo.– Wao waliifukizia ubani miungu yao kwenye milima, wakanitukana mimi kule juu ya vilima. Nitawalipa sawa inavyostahili, watayalipa matendo yao ya zamani. Yawe anasema hivi: Mutu akikuta kishada cha mizabibu mizuri, watu wanasema: Tusikiharibu; kina baraka. Ndivyo nitakavyofanya kwa ajili ya watumishi wangu; sitawaangamiza wote. Nitawajalia watu wa Yakobo, na Yuda nitamujalia watakaorizi milima yangu; wachaguliwa wangu watairizi, watumishi wangu watakaa kule. Bonde la Saroni litakuwa nafasi ya kukulishia nyama, bonde la Akori litakuwa mapumziko ya ngombe kwa ajili ya watu wangu walionitafuta. Lakini nitafanya nini na ninyi munaoniacha mimi Yawe, musioujali Sayuni, mulima wangu mutakatifu, munaotolea miungu chakula na divai kusudi iwapatie bahati zuri. Nimewapangia kifo kwa upanga, ninyi wote mutanaswa kwa kuchinjwa! Maana, nilipowaita, hamukuniitikia; niliposema, hamukunisikiliza. Mulitenda maovu mbele yangu, mukachagua yale nisiyoyapenda. Basi, mimi Yawe ninasema: Watumishi wangu watakula, lakini ninyi mutasikia njaa; watumishi wangu watakunywa, lakini ninyi mutasikia kiu; watumishi wangu watafurahi, lakini ninyi mutafezeheka. Watumishi wangu wataimba kwa furaha ndani ya moyo, lakini ninyi mutalia kwa uchungu ndani ya moyo na kupiga kelele kwa uchungu mukubwa ndani ya roho. Wale niliowachagua nitawapa jina jipya. Lakini ninyi jina lenu watalitumia kwa kulaani; watasema: Bwana wetu Yawe awaue. Basi, mwenye kujitakia baraka katika inchi, atajitakia baraka kwa Mungu wa kweli. Mwenye kuapa katika inchi hii, ataapa kwa Mungu wa kweli. Maana taabu za zamani zimepita zimetoweka kabisa mbele yangu. Sasa, ninaumba mbingu mupya na dunia mupya. Mambo ya zamani hayatakumbukwa tena. Mufurahi na kushangilia milele, kwa ajili ya vitu hivi ninavyoumba. Yerusalema nitaifanya muji wa shangwe, na watu wake watu wenye furaha. Nami nitaufurahia Yerusalema, nitawafurahia watu wangu. Sauti ya kilio haitasikilika tena, kilio cha taabu hakitakuwa tena. Hakutakuwa tena vifo vya watoto wachanga, wazee nao hawatakufa mbele ya wakati wao. Mutu wa miaka mia moja akikufa, amekufa akiwa kijana; na akikufa mbele ya miaka mia moja, ni kusema amelaaniwa. Watu watajenga nyumba na kuishi humo; watalima mizabibu na kula matunda yake. Hawatajenga nyumba na watu wengine wakae ndani yake, wala kulima chakula kikuliwe na watu wengine. Maana watu wangu niliowachagua wataishi maisha marefu kama miti; wachaguliwa wangu watafurahia matunda ya jasho lao. Kazi zao hazitakuwa bure, wala hawatazaa watoto watakaopatwa na musiba; maana watakuwa waliobarikiwa na Yawe, wamebarikiwa wao pamoja na wazao wao. Hata mbele hawajaniita, mimi nitawaitikia; mbele hawajamaliza kusema, nitakuwa nimewajibu. Imbwa wa pori na kondoo watakula pamoja, simba watakula majani kama ngombe, lakini chakula cha nyoka kitakuwa mavumbi. Katika mulima wangu wote mutakatifu, hakuna atakayeumiza au kuharibu kitu. –Ni Yawe anayesema hivyo. Yawe anasema hivi: Mbingu ni kiti changu cha kifalme, dunia ni kiti cha kupumzikishia miguu yangu. Mutanijengea nyumba ya namna gani basi, pahali nitakapoweza kupumzikia? Mimi mwenyewe nilivifanya vitu hivi vyote, na hivi vyote ni mali yangu. Lakini ninachojali mimi, ni mutu munyenyekevu na mwenye moyo wenye kuvunjika, mutu anayetetemeka anaposikia neno langu. –Ni ujumbe wa Yawe. Lakini watu hawa wanafanya wanavyotaka: wananitolea sadaka ya ngombe na tena wanaua watu kwa kutambikia. Wananitolea sadaka ya mwana-kondoo na vilevile wanaua imbwa. Wananitolea sadaka ya unga na vilevile wanatolea damu ya nguruwe. Wanachoma ubani mbele yangu na kwenda kuabudu miungu ya uongo. Hao wamechagua kufuata njia zao wenyewe. Basi, nitawaletea taabu; zile hasara zote wanazoogopa zitawapata; maana nilipoita hakuna aliyeitika, niliposema hawakunisikiliza. Lakini walifanya maovu mbele yangu, walichagua yale ambayo hayanipendezi. Musikilize neno la Yawe, enyi munaotetemeka kwa sababu ya neno lake. Wandugu zenu ambao wanawachukia, na kuwafukuza kwa sababu yangu, wamesema hivi kwa kuwachekelea: Mungu aonyeshe utukufu wake, nasi tuwaone ninyi mukishinda! Lakini wao wenyewe ndio watakaopata haya! Musikilize: makelele kutoka katika muji, sauti kutoka katika hekalu! Hiyo ni sauti ya Yawe akiwaazibu waadui zake! Muji wangu mutakatifu, ni kama mama anayezaa bila kupata uchungu; mbele ya uchungu kuanza, amekwisha zaa mutoto. Ni nani aliyepata kusikia jambo kama lile? Ni nani aliyepata kuona jambo kama lile? Inchi nzima inaweza kuzaliwa kwa siku moja? Taifa zima linaweza kuzaliwa kwa mara moja? Maana mara moja tu Sayuni ulipoanza kupata uchungu, palepale ukazaa watoto wake. Namna gani ninaweza kumufikisha mutoto kwa saa ya kuzaliwa, halafu nimuzuize asizaliwe? –Ni Yawe anayesema hivyo.– Au mimi mwenye kuwajalia watoto, namna gani nitafunga uzazi? –Ni Mungu wenu anayesema hivyo. Mushangilie na kufurahi pamoja na Yerusalema, enyi munaoupenda! Mushangilie pamoja nao, enyi wote mulioulilia! Hivi mutapata kunyonya, nanyi mutashiba kwa riziki zake; mutayakunywa na kufurahi, kutokana na wingi wa utukufu wake. Maana Yawe anasema hivi: Nitakuletea fanaka nyingi kama muto, utajiri wa mataifa kama muto uliofurika. Nanyi mutanyonya na kubebwa kama mutoto muchanga, mutabembelezwa kama mutoto juu ya magoti ya mama yake. Kama vile mama anavyomufariji mwana wake, vilevile nami nitawafariji; mutafarijiwa katika Yerusalema. Mutayaona hayo na mioyo yenu itafurahi; mifupa yenu itastawi tena kama vile majani mabichi. Kwa hiyo itajulikana kwamba mimi Yawe ninawalinda watumishi wangu, lakini nikikasirika ninawaazibu waadui zangu. Yawe atakuja kama moto, na magari yake ya vita ni kama zoruba. Ataiacha hasira yake ifanye kazi yake kwa ukali, na maonyo yake yatimizwe kwa ndimi za moto. Yawe atatoa hukumu kwa moto atawaazibu watu wote kwa upanga; nao atakaowaangamiza watakuwa wengi. Kuna watu wanaojitakasa na kujisafisha wapate kuingia kwenye bustani za ibada za sanamu; wanafanya maandamano na kuhani akiwa kati yao. Watu wale wanakula nguruwe, panya na vyakula vingine vyenye kuwa machukizo. Watu wale hakika watakufa wote pamoja. –Ni ujumbe wa Yawe.– Ninayajua matendo yao na mawazo yao. Ninakuja kuwakusanya watu wa mataifa yote na wa luga zote, wakusanyike pamoja na kuuona utukufu wangu. Nitaweka kati yao kitambulisho cha uwezo wangu. Watakaookolewa kati yao nitawapeleka kwa watu wa mataifa kule Tarsisi, Puti, Ludi, inchi zenye wafundi wa kupiga upinde; watakwenda vilevile Tubali na Ugriki na katika visanga vya mbali ambapo watu hawajapata kusikia habari zangu wala kuuona utukufu wangu. Wale wajumbe wangu watautangaza utukufu wangu katika mataifa hayo. Watawarudisha wandugu zenu wote kutoka katika mataifa yote kama matoleo yangu mimi Yawe. Watawaleta juu ya farasi, juu ya nyumbu, juu ya ngamia na ndani ya magari na juu ya vipoyi mpaka Yerusalema, kwenye mulima wangu mutakatifu. Watawaleta kama Waisraeli wanavyoleta sadaka ya unga katika chombo safi mpaka ndani ya nyumba yangu mimi Yawe. Vilevile nitawachagua wamoja kati yao kuwa makuhani na Walawi. –Ni Yawe anayesema hivyo. Kama vile mbingu mupya na dunia mupya nitakazoumba zitakavyodumu milele kwa uwezo wangu, ndivyo wazao wako na jina lako litakavyodumu. –Ni ujumbe wa Yawe.– Katika kila sikukuu ya mwandamo wa mwezi, na katika kila siku ya Sabato, wanadamu wote watakuja kuniabudu. –Ni Yawe anayesema hivyo. Kisha watakwenda kuziona maiti za wale walioniasi. Wadudu watakaowakula hawatakufa, na moto utakaowachoma hautazimika hata kidogo. Watakuwa chukizo kwa watu wote. Maneno ya Yeremia mwana wa Hilkia, mumoja wa makuhani wa muji Anatoti, katika inchi ya kabila la Benjamina. Neno la Yawe lilimufikia Yeremia katika mwaka wa kumi na tatu wa utawala wa Yosia mwana wa Amoni, mufalme wa Yuda. Tena lilimufikia Yeremia wakati Yoyakimu mwana wa Yosia, alipokuwa mufalme wa Yuda. Neno la Yawe liliendelea kumufikia mpaka mwisho wa mwaka wa kumi na mumoja wa utawala wa Zedekia, mwana wa Yosia, mufalme wa Yuda. Ni katika mwezi wa tano wa mwaka huo, ndio wakati watu wa Yerusalema walipelekwa katika uhamisho. Neno la Yawe lilinifikia kusema hivi: Mbele ya kukutengeneza katika tumbo la mama yako, mimi nilikujua; mbele haujatoka katika tumbo, nilikuweka kwa kazi yangu; mimi nilikuchagua kuwa nabii kwa mataifa. Nami nikajibu: Ee! Bwana wangu Yawe, mimi sijui kusema, ningali bado kijana. Lakini Yawe akaniambia: Usiseme kwamba ungali kijana. Utakwenda kwa watu ninaokutuma kwao, na maneno yote nitakayokuamuru, utayasema. Wewe usiwaogope watu hao. Niko pamoja nawe kwa kukulinda. –Ni ujumbe wa Yawe. Kisha Yawe akanyoosha mukono wake, akagusa kinywa changu, akaniambia: Nimetia maneno yangu ndani ya kinywa chako. Leo nimekupa mamlaka juu ya mataifa na falme, ukuwe na mamlaka ya kuongoa na kubomoa, mamlaka ya kuharibu na kuangamiza, mamlaka ya kujenga na ya kupanda mbegu. Neno la Yawe lilinifikia kusema hivi: Yeremia, unaona nini? Nami nikasema: Ninaona tawi la muti wa uangalivu ambao maua yake yamekwisha kuchanua. Yawe akaniambia: Umeona vizuri, kwa maana nitakuwa na uangalivu kusudi maneno yangu yapate kutimia. Neno la Yawe lilinifikia mara ya pili kusema hivi: Unaona nini? Nami nikasema: Ninaona chungu kinachotokota, nacho kinainamia upande wangu tokea kaskazini. Yawe akaniambia: Maangamizi yataanzia tokea kaskazini na kuwapata wakaaji wote wa inchi hii. Maana ninaziita falme zote na makabila yote ya kaskazini. Wafalme wake wote watakuja na kila mumoja wao ataweka kiti chake cha kifalme mbele ya milango ya ukuta wa Yerusalema na kandokando ya kuta zake zote, na kuizunguka miji yote ya Yuda. Nami nitawahukumu Waisraeli kwa ajili ya uovu wao wote, kwa maana waliniacha mimi na kuifukizia miungu mingine ubani na kuabudu sanamu walizojitengenezea wenyewe. Sasa basi, wewe Yeremia ujiweke tayari. Simama! Uende kuwaambia mambo yote ninayokuamuru. Usiwaogope, kusudi mimi nisikufanye kuwa mwoga mbele yao. Na tangu leo, ninakufanya kuwa imara kama muji unaozungukwa na kuta, kama munara wa chuma na kama ukuta mugumu sana wa shaba. Utakuwa na nguvu juu ya inchi yote, juu ya wafalme wa Yuda, wakubwa wake, makuhani wake na watu wake wote. Watapigana nawe, lakini hawatashinda, kwa sababu mimi niko pamoja nawe kwa kukuokoa. –Ni ujumbe wa Yawe. Neno la Yawe lilinifikia kusema hivi: Kwenda uwatangazie waziwazi wakaaji wote wa Yerusalema na kusema hivi: Yawe anasema hivi: Ninakumbuka wema wako ulipokuwa kijana, jinsi ulivyonipenda kama muchumba wako. Ulinifuata katika jangwa kwenye inchi ambayo haikupandwa kitu. Israeli, ulikuwa wangu wa pekee, kama malimbuko ya shamba langu. Wote waliokukula walibeba hukumu, wakipatwa na hasara. –Ni ujumbe wa Yawe. Musikilize neno la Yawe, enyi wazao wa Yakobo. Musikilize, enyi jamaa zote za wazao wa Israeli. Yawe anasema hivi: Babu zenu waliona kosa gani kwangu hata wakanigeuka na kuniacha, wakakimbilia miungu ya bure, hata nao wakakuwa watu bure? Hawakujiuliza hivi: Yuko wapi Yawe aliyetuondoa katika inchi ya Misri, aliyetuongoza katika mbuga, katika inchi ya jangwa na mashimo, inchi inayokauka na yenye giza kubwa, inchi isiyopitiwa na mutu yeyote, wala kukaliwa na mwanadamu? Niliwaleta katika inchi yenye mboleo, muyafurahie mazao yake na mema yake mengine. Lakini mulipofika tu, muliichafua inchi yangu; inchi niliyowapa ikuwe yenu, mukaifanya chukizo. Nao makuhani hawakujiuliza hivi: Yuko wapi Yawe? Wafundi wa sheria hawakunijua, viongozi wa watu waliniasi; manabii nao walitabiri kwa jina la Bali na kuabudu sanamu zisizokuwa na faida yoyote. Kwa hiyo, mimi nitawashitaki ninyi, na nitawashitaki wazao wenu. –Ni ujumbe wa Yawe.– Basi muvuke bahari mpaka Kipuro, muone, au mutume watu huko Kedari wachunguze, kama jambo kama hili limekwisha kutokea. Kuna taifa ambalo limekwisha kubadilisha miungu yao ingawa miungu hiyo si miungu? Lakini watu wangu wameniacha mimi, utukufu wao, wakafuata miungu isiyokuwa na faida yoyote. Kwa hiyo mushangae, enyi mbingu, muogope na kufazaika kabisa. –Ni ujumbe wa Yawe.– Watu wangu wametenda maovu mawili; wameniacha mimi ninayekuwa chemichemi ya maji ya uzima, wakajichimbia visima vyao wenyewe, visima vyenye nyufa, visivyoweza kuchunga maji. Israeli ni mutumwa, au amezaliwa mutumwa? Hapana! Kwa nini basi amekuwa kama nyama anayewindwa? Simba wananguruma kwa ajili yake, wananguruma kwa sauti kubwa. Wameiharibu kabisa inchi yake, miji yake imebaki mabomoko pasipo watu. Hata watu wa Nofi na Tahapanesi, wamenyoa nywele ya kichwa chake. Israeli, si wewe mwenyewe uliyejiletea hayo yote, kwa kuniacha mimi Yawe, Mungu wako, niliyekuwa ninakuongoza katika njia? Na sasa itakufalia nini kwenda Misri kunywa maji ya muto Nili? Au itakufalia nini kwenda Asuria kunywa maji ya muto Furati? Uovu wako utakuazibu; na uasi wako utakuhukumu. Ujue na kutambua kwamba ni vibaya sana kuacha Bwana wako Yawe, Mungu wako, na kutokuwa na woga wangu ndani yako. –Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe wa majeshi.– Yawe anasema: Tangu zamani wewe ulivunja nira yako, ulikata minyororo yako, ukasema: “Sitakutumikia”. Juu ya kila kilima kirefu na chini ya kila muti wa majani mabichi, ukalala machali kama kahaba. Lakini mimi nilikupanda kama mizabibu uliochaguliwa, muzabibu wenye afya na wa mbegu safi. Mbona basi umeharibika, umegeuka kuwa muzabibu wa bure wa pori? Hata ukijisafisha kwa dawa ya kutosha taka na kutumia sabuni nyingi, madoa ya uovu wako yatabaki mbele yangu. –Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe. Namna gani basi unaweza kusema: Mimi sikujichafua wala sikufuata miungu Bali. Ukumbuke vile ulivyotenda zambi kule katika bonde; utambue yale uliyofanya huko! Wewe ni kama mwana wa ngamia, anayetangatanga huko na huko; kama punda dike wa pori aliyezoea jangwa. Katika tamaa yake ananusanusa upepo; nani anayeweza kumuzuiza katika hamu yake? Dume anayemutamani hahitaji kujisumbua; wakati wake unapofika watamupata tu. Israeli, usiichubue miguu yako wala usilikaushe koo lako. Lakini wewe unasema: Hakuna tumaini lolote. Ninapenda miungu ya kigeni, hiyo ndiyo nitakayoifuata. Kama vile mwizi anavyofezeheka anaponaswa, ndivyo Waisraeli watakavyofezeheka; wao wenyewe, wafalme wao, wakubwa wao, makuhani wao na manabii wao. Wao wanauambia muti: “Wewe ni baba yetu”, nalo jiwe: “Wewe ndiwe uliyetuzaa”; kwa maana unanigeuzia mugongo, wala hawakunielekezea uso. Lakini wakati wa shida wanasema: Simama utuokoe! Lakini iko wapi ile miungu yenu muliyojifanyia? Basi kama inaweza, isimame iwasaidie, wakati munapokuwa katika shida. Ee ninyi watu wa Yuda, hesabu ya miungu yenu ni sawa na hesabu ya miji yenu! Kwa nini basi munanilalamikia? Ninyi wote mumeniasi. –Ni ujumbe wa Yawe.– Niliwaazibu ninyi lakini ilikuwa bure, ninyi munakataa maonyo. Muliwateketeza manabii wenu kwa upanga kama simba mwenye uchu. Enyi watu! Musikilize vile mimi Yawe ninavyosema: Nimekuwa kama vile jangwa au inchi yenye giza kubwa? Kwa nini basi watu wangu wanasema: Sisi tuko watu huru; hatutakurudilia! Kijana binti anaweza kusahau mapambo yake, au bibi arusi nguo yake? Lakini watu wangu wamenisahau kwa muda wa siku zisizohesabika. Kweli wewe ni bingwa wa kutafuta wapenzi! Hata wanawake waovu unawafundisha njia zako. Juu ya nguo zako kuna damu ya wamasikini wasiokuwa na kosa, ijapokuwa haukuwakuta wakivunja nyumba yako. Na zaidi ya hayo yote, wewe unasema: Mimi sina kosa; hakika hasira yake imegeuka mbali nami. Lakini mimi nitakuhukumu kwa sababu unasema kwamba haukutenda zambi. Kwa nini unaniachilia hivi, ukibadilishabadilisha mwenendo wako? Utafezeheshwa na Misri kama ulivyofezeheshwa na Asuria. Na huko vilevile utatoka na haya, mikono ikiwa juu ya kichwa. Mimi Yawe nimewakataa wale uliowategemea, wala hautafanikiwa kwa musaada wao. Mume akiachana na muke wake, naye muke akijiendea, na kuolewa na mwingine, mume yule anaweza kumurudilia muke huyo? Kufanya hivyo hakutaichafua inchi kabisa? Wewe Israeli, umefanya ukahaba na wapenzi wengi, sasa unataka kunirudilia mimi? –Ni ujumbe wa Yawe.– Inua macho, uangalie vilele vya vilima! Kuna nafasi ambapo hawajalala nawe? Uliwangoja wapenzi wako kando ya njia, kama mubedui anavyovizia watu katika jangwa. Umeichafua inchi kwa ukahaba wako mubaya sana. Ndiyo maana manyunyu yamezuizwa kuanguka, wala mvua za mwisho hazijanyesha. Hata hivyo unakausha macho kama kahaba, wala hauna haya hata kidogo. Na sasa hivi tu unanililia, ukisema: Wewe ni baba yangu, ulinipenda tangu utoto wangu? Utanikasirikia siku zote? Utachukizwa nami milele? Israeli, vile ndivyo unavyosema; na kumbe umetenda uovu wote ulioweza. Katika siku ya utawala wa mufalme Yosia, Yawe aliniambia hivi: Umeona jinsi yule Israeli asiyekuwa mwaminifu alivyofanya? Aliniacha, akapanda juu ya kila kilima kirefu na kwenda chini ya kila muti wenye majani mabichi, akafanya ukahaba wake kule! Mimi nilizani kwamba nyuma ya kufanya hayo yote, atanirudilia. Lakini hakunirudilia. Yuda, dada yake mudanganyifu, alishuhudia hayo yote. Zaidi ya hayo, Yuda alishuhudia kwamba niliachana na Israeli kwa sababu ya ukahaba wake na kwa kukosa uaminifu kwangu. Lakini hata hivyo, Yuda, dada yake mudanganyifu, hakuogopa; naye vilevile alikwenda na kufanya ukahaba! Aliona kwamba ukahaba ni jambo dogo sana kwake. Aliichafua inchi kwa kufanya ukahaba, akiabudu mawe na miti. Pamoja na hayo yote, Yuda, dada mudanganyifu wa Israeli hakunirudilia kwa moyo wote, lakini kwa unafiki tu. –Ni ujumbe wa Yawe. Yawe akaendelea kuniambia hivi: Muasi Israeli amejionyesha kuwa wa haki kuliko Yuda mudanganyifu. Basi, kwenda umutangazie Israeli maneno haya: Rudi, ewe Israeli usiyekuwa mwaminifu. –Ni ujumbe wa Yawe.– Nami sitakuangalia kwa hasira maana mimi ni mwema. –Ni ujumbe wa Yawe.– Kweli, sitakukasirikia milele. Wewe, kubali tu kosa lako: kwamba umeniasi mimi Yawe, Mungu wako; kwamba chini ya kila muti wenye majani, umeonyesha mapenzi yako kwa miungu mingine, wala haukuitii sauti yangu. –Ni ujumbe wa Yawe. Murudi, enyi watoto musiokuwa na uaminifu, maana, mimi ndimi Bwana wenu. Nitawatwaa mumoja kutoka kila muji, na wawili kutoka katika kila ukoo, niwapeleke mpaka kwenye mulima Sayuni. –Ni ujumbe wa Yawe. Nitawapa wachungaji wanaopendeza moyo wangu, watakaowakulisha kwa akili. Siku hizo, wakati mutakapokuwa mumeongezeka na kuwa wengi katika inchi, watu hawatalitajataja tena Sanduku langu la Agano. –Ni ujumbe wa Yawe.– Hawatalifikiri juu yake kabisa, wala hawatalikumbuka tena; hawatalihitaji, wala hawatatengeneza lingine. Wakati huo, Yerusalema utaitwa “Kiti cha Kifalme cha Yawe”, na mataifa yote yatakusanyika humo mbele yangu. Hawatafuata tena ugumu wao unaotokana na matendo yao mabaya. Siku hizo, watu wa Yuda wataungana na watu wa Israeli, na wote kwa pamoja watatoka katika inchi ya kaskazini na kurudi katika inchi niliyowapa babu zenu ikuwe urizi wao. Yawe anasema: Wewe Israeli, mimi niliwaza hivi: heri ningekuhesabia kati ya wana wangu, na kukupa inchi nzuri ajabu, ndio urizi unaopita inchi zote za mataifa. Nilizani utaniita Baba Yako, na kwamba haungeacha kunifuata. Lakini kama muke asiyekuwa mwaminifu anavyomwacha mume wake, ndivyo ulivyokosa uaminifu kwangu. –Ni ujumbe wa Yawe. Kelele linasikilika juu ya vilima: Waisraeli wanalia na kuomboleza, kwa sababu wamepotoka katika njia zao, wamenisahau mimi Yawe, Mungu wao. Murudi, enyi watoto musiokuwa na uaminifu, mimi nitawaponyesha ukosefu wenu wa uaminifu. Nanyi munasema: Sisi tunarudi kwako, maana wewe ndiwe Yawe, Mungu wetu. Kweli tumedanganyika sana kwa kutambikia huko kwenye vilima, hakika wokovu wa Israeli unatoka kwake Yawe, Mungu wetu. Tangu ujana wetu, tendo hili la haya limeangamiza kila kitu babu zetu walichokitoshea jasho: makundi yao ya kondoo na ngombe, wana wao na wabinti zao. Sherti tujilaze chini kwa ajili ya haya, na kujiachilia kufunikiwa na haya yetu. Tangu ujana wetu mpaka leo hii, sisi wenyewe, kama vile babu zetu, tumetenda zambi mbele ya Yawe, Mungu wetu, wala hatukumutii Yawe, Mungu wetu. Yawe anasema hivi: Ukitaka kurudi, ee Israeli, unirudilie mimi. –Ni ujumbe wa Yawe.– Ukiviondoa vitu vyako vya kuchukiza mbele yangu, usipotangatanga huko na huko, ukiapa kwa ukweli, kwa kufuatana na sheria, na kwa haki, kwa kusema “Kama vile Yawe anavyoishi”, halafu mataifa yatapata baraka kutoka kwangu, na kutukuzwa kwa sababu yangu. Yawe anawaambia hivi watu wa Yuda na wakaaji wa Yerusalema: Mulime mashamba yenu mapya; musipande mbegu zenu penye miiba. Enyi watu wa Yuda na wakaaji wa Yerusalema, mujitahiri, mukiondoa govi za mioyo yenu, mupate kujitoa kwa Yawe. Kama si vile, kasirani yangu itawaka kama moto, nayo itaunguza wala hakuna atakayeizimisha, kwa sababu ya matendo yenu maovu. Mutoe tangazo, mupashe habari huko Yerusalema! Mupige baragumu kila pahali katika inchi! Mulalamike, mukisema: Mukusanyike pamoja! Mukimbilie katika miji yenye kuzungukwa na kuta! Muinue bendera ya vita kuelekea Sayuni, kusudi mukimbie, wala musisitesite! Yawe analeta hasara, analeta maangamizi makubwa kutoka kaskazini. Kama simba anavyotoka kwenye maficho yake, mwangamizaji wa mataifa ameanza kuja, anakuja kutoka pahali pake, kusudi aharibu inchi yenu. Miji yenu itabaki mabomoko matupu, bila kukaliwa na mutu yeyote. Kwa hiyo, muvae gunia, muomboleze na kulia; kwa maana Yawe hajaondoa hasira yake kali kwenu. Siku hiyo, mufalme na wakubwa wataregea moyo. Makuhani watapigwa na bumbuazi, na manabii watashangaa. –Ni ujumbe wa Yawe. Kisha nikasema: Ee, Bwana wangu Yawe, hakika umewadanganya kabisa watu hawa, nao Yerusalema! Uliwaambia mambo yataongoka vizuri kwao, kumbe maisha yao yako katika hatari kabisa! Wakati huo, wataambiwa hivi watu hawa pamoja na muji Yerusalema: Upepo wenye kuunguza kutoka vilele vya milima katika jangwa utawavumia watu wangu. Huo si upepo mudogo wa kupepeta ngano, lakini ni upepo mukali sana unaotoka kwangu. Ni mimi Yawe nitakayetoa hukumu juu yao. Angalia! Adui anakuja akivuma kama mawingu. Magari yake ya vita ni kama zoruba, nao farasi wake wa vita wanaruka mbio kuliko tai. Ole kwetu! Tumeangamia! Wewe Yerusalema, usafishe maovu ya moyo wako, kusudi upate kuokolewa. Mpaka wakati gani utaendelea kuchunga maovu? Sauti kutoka Dani inatoa tangazo; inatangaza hasara kutoka vilima vya Efuraimu. Inayaarifu mataifa, inaitangazia Yerusalema maneno haya: Washambulizi wanakuja kutoka inchi ya mbali, wanaitisha miji ya Yuda, wanauzunguka Yerusalema kama walinzi wanavyozunguka mashamba, kwa sababu watu wake wameniasi. –Ni ujumbe wa Yawe. Wewe Yuda, hayo yote yamekupata kwa ajili ya mwenendo na matendo yako. Hiyo ndiyo hasara inayokufikia, tena ni yenye uchungu; yamepenya mpaka ndani ya moyo wako. Uchungu, uchungu! Ninagaagaa kwa uchungu! Moyo wangu unapigapiga vibaya. Wala siwezi kukaa kimya. Maana ninaogopa mulio wa baragumu, ninasikia kelele la vita. Wanatangaza hasara zisizokoma; inchi yote imeharibiwa. Kwa rafla mahema yetu yameharibiwa, mapazia yao yamepasuka kwa dakika moja. Mpaka wakati gani nitaendelea kuona bendera za vita na kusikia mulio wa baragumu? Yawe anasema: Watu wangu ni wapumbafu, hawanijui mimi. Wao ni watoto wajinga; hawana ufahamu. Wao wanaelewa vizuri kutenda maovu, lakini hawajui kutenda mema. Niliangalia dunia, nikaona imekuwa ukiwa na tupu; niliangalia mbingu, nazo hazikukuwa na mwangaza. Niliangalia milima, nikaiona ikitetemeka, navyo vilima vyote vilikuwa vikiyumbayumba. Niliangalia wala sikuona mutu; hata ndege katika anga walikuwa wametoweka. Niliona inchi yote yenye mboleo imegeuka jangwa, nayo miji yake yote imebaki mabomoko matupu, kwa sababu ya hasira kali ya Yawe. Maana Yawe anasema hivi: Inchi nzima itakuwa jangwa tupu; lakini sitaiharibu kabisa. Kwa hiyo, inchi itaomboleza, na mbingu zitakuwa nyeusi. Maana nimesema nami sitabadilisha nia yangu; nimeamua, wala sitarudi nyuma. Kelele la waaskari wapanda-farasi na la wapiga mishale litakaposikilika, watu wote watakimbia. Wamoja wao watakimbilia katika vichaka, wengine watajificha katikati ya mawe. Kila muji utaachwa tupu; hakuna mutu atakayekaa ndani yake. Nawe Yerusalema uliyeachwa tupu, kwa nini sasa unavaa nguo nzuri nyekundu? Kwa nini kujipamba kwa zahabu, na kujipakaa wanja kwenye macho? Unajipamba bure! Wapenzi wako wanakuzarau sana; wanatafuta kukuua tu. Nilisikia sauti kama ya mwanamuke anayezaa, malalamiko kama ya mwenye kuzaa mutoto wa kwanza. Ilikuwa sauti ya Yerusalema akipumuapumua kwa uchungu, na kuinyooshanyoosha mikono yake, akisema: Ole wangu! Wanakuja kuniua! Mukimbie huko na huko katika Yerusalema, mupeleleze na kujionea wenyewe, muchunguze katika masoko yake. Mukiona hata mutu mumoja anayefuata sheria, mutu anayetafuta ukweli, basi Yawe atausamehe Yerusalema. Ingawa watu wake wanaapa kwa nafsi ya Yawe, viapo vyao ni vya uongo. Ee Yawe, wewe unatafuta uaminifu siku zote. Umewatwanga, lakini hawakuona uchungu; umewateketeza, lakini walikataa maonyo. Wamevifanya vichwa vyao kuwa vigumu kuliko jiwe; wamekataa kabisa kurudi kwako. Kwa hiyo niliwaza hivi: Watu hawa ni zaifu, hawana akili; hawajui mapenzi ya Yawe, hawajui Sheria ya Mungu wao. Nitawaendea wakubwa niongee nao; bila shaka, wao wanajua mapenzi ya Yawe; wanajua sheria ya Mungu wao. Lakini wote ni sawa. Wamevunja nira yao, wamekata minyororo yao. Kwa hiyo simba kutoka pori atawaua; imbwa wa pori kutoka jangwa atawararua. Chui anaivizia miji yao. Kila mutu anayetoka humo atararuliwa vipandevipande, kwa sababu zambi zao ni nyingi, maasi yao ni makubwa. Yawe anauliza: Namna gani nitaweza kukusamehe, ee Yerusalema? Watu wako wameniasi; wameapa kwa majina ya miungu ya uongo. Nilipowashibisha kwa chakula, wao walifanya uzinzi, wakakusanyika kwa uwingi katika nyumba za makahaba. Walikuwa kama farasi dume wanono wenye tamaa, kila mumoja anamutamani muke wa jirani yake. Basi, nisiwaazibu kwa ajili ya mambo haya yote? –Ni ujumbe wa Yawe.– Nisilipize kisasi juu ya taifa kama hili? Mupande, mupite katika mashamba yake ya mizabibu, muharibu kila kitu lakini musivimalize kabisa. Mukate matawi yake, kwa maana hayo si yangu mimi Yawe. Kweli, watu wa Israeli na watu wa Yuda, wamekosa kabisa uaminifu kwangu. –Ni ujumbe wa Yawe.– Watu hao wamesema uongo juu ya Yawe. Wamesema: Hatafanya kitu; hatutapatwa na hasara yoyote; hatutafikiwa na vita wala njaa. Manabii si kitu, ni upepo tu. Maneno wanayoyasema hayatoki kwa Mungu. Iwatokee kama vile wanavyosema! Yawe wa majeshi anasema hivi: Kwa sababu wao wamesema jambo hilo, sasa nitayafanya maneno niliyokupa wewe Yeremia kuwa moto. Nao watu hawa watakuwa kuni, na moto huo utawateketeza. Na kwa ngambo yenu ninyi watu wa Israeli, ninaleta taifa moja kutoka mbali kuwashambulia. –Ni ujumbe wa Yawe.– Hili taifa haliwezi kushindwa, ni taifa la zamani, ni taifa ambalo hamufahamu luga yake. Hamuwezi kuelewa hata neno wanalolisema. Mishale yao inaua watu kwa uwingi, wote ni mashujaa wa vita. Watakula mazao yenu na chakula chenu; watawaua wana na wabinti zenu. Watachinja makundi yenu ya kondoo na ngombe; wataiharibu mizabibu yenu na miti yenu ya matunda ya tini. Miji yenu yenye kuzungukwa na kuta munayoitegemea, wataiharibu kwa silaha zao. Lakini hata katika siku hizo mimi, sitawaangamiza ninyi na kuwamaliza kabisa. –Ni ujumbe wa Yawe. Na watu wenu watakapouliza: Kwa nini Yawe, Mungu wetu, ametutendea mambo hayo yote? Wewe Yeremia utawajibu hivi: Ninyi mulimwacha Yawe, mukaitumikia miungu ya kigeni katika inchi yenu. Basi ndivyo mutakavyowatumikia watu wengine katika inchi isiyokuwa yenu. Muwatangazie wazao wa Yakobo; muwaambie hao watu wa Yuda hivi: Musikilize, enyi wajinga na wapumbafu: ninyi munaokuwa na macho, lakini hamwoni, munaokuwa na masikio, lakini hamusikii. Mbona hamuniogopi? –Ni ujumbe wa Yawe.– Kwa nini hamutetemeki mbele yangu? Mimi niliwekea bahari muchanga kuwa mupaka wake; ni kizuizo cha milele ambacho bahari haiwezi kuvuka. Ingawa mawimbi yanaupiga, hayawezi kuupita; ingawa yanavuma, hayawezi kuuruka. Lakini watu hawa wana moyo mugumu na wa uasi; wamegeuka na kuniacha. Wala hawasemi wenyewe hivi: Inatupasa kumwogopa Yawe, Mungu wetu, anayetujalia mvua kwa wakati wake, anayetupatia mvua za kwanza na mvua za mwisho; na kutupatia nyakati nzuri za mavuno. Makosa yenu yamewazuia musipate baraka hizo, zambi zenu zimewafungia kupata mema yale. Hakika, kati ya watu wangu kuna waovu, watu ambao wananyanganya mali za wengine. Wako kama wawindaji wa ndege: wanatega mitego yao na kuwanasa watu. Kama vile kikapu kinachojaa ndege walionaswa, ndivyo nyumba zao zinavyojaa mali za udanganyifu. Ndiyo maana wamekuwa watu wakubwa na watajiri, wamenenepa na kungaa vizuri. Maovu yao hayana mwisho, hawahukumu yatima kwa kufuatana na sheria kusudi wapate kufanikiwa, wala hawatetei haki za watu wakosefu. Mimi sitawaazibu kwa ajili ya mambo haya? Nitaachilia taifa hili bila kulilipiza kisasi? –Ni ujumbe wa Yawe. Jambo la ajabu na la kuchukiza limetendeka katika inchi hii: manabii wanatabiri mambo ya uongo, nao makuhani wanatafuta faida yao wenyewe; nao watu wangu wanaona jambo hilo kuwa sawa. Lakini mwisho wake utakapofika mutafanya nini? Enyi watu wa kabila la Benjamina, muondoke Yerusalema, mukimbie! Mupige baragumu katika muji Tekoa! Muonyeshe kitambulisho cha vita huko Beti-Keremu, maana hasara na maangamizi makubwa vinakuja kutoka upande wa kaskazini. Muji wa Sayuni ni muzuri na wenye kupendeza, lakini utaharibiwa. Watu wataufikia kama vile wachungaji na makundi yao, watasimamisha hema zao kandokando yake, kila wamoja upande wao kwa kulisha makundi yao. Halafu watasema: Mujitayarishe, tupigane vita na Sayuni. Musimame, tuushambulie pa saa sita za muchana! Bahati mbaya kwetu, maana jua linatua! Saa za magaribi zinakaribia. Basi, tutaushambulia usiku; tutaziharibu nyumba zake nzuri zote. Yawe wa majeshi anasema hivi: Mukate miti na kulundika udongo, kwa kuweza kupandia ndani ya Yerusalema. Muji huu unapaswa uazibiwe, maana hamuna lolote ndani yake isipokuwa ukorofi tu. Kama vile maji yanavyotiririka toka ndani ya kisima, ndivyo maovu yanavyotiririka katika Yerusalema. Mateso makali na maangamizi yanasikilika ndani yake. Ninaona magonjwa na vidonda mbele yangu kila siku. Basi usikilize maonyo, ee Yerusalema. Kama sivyo nitakutupilia mbali; nitakufanya ukuwe jangwa, kuwa pahali pasipokaliwa na mutu. Yawe wa majeshi anasema hivi: Muwakusanye watu wote wa Israeli waliobaki kama vile watu wanavyookotesha zabibu katika shamba; kama vile muchumaji wa zabibu, mupitishe mikono katikati ya matawi yote. Nitaongea na nani nipate kumwonya, kusudi wapate kunisikia? Angalia, masikio yao yameziba, hawawezi kusikia ujumbe wako. Maneno ya Yawe, yamegeuka kwao jambo la kuchekelea. Hawalifurahii hata kidogo. Nimejaa hasira ya Yawe nami ninachoka kwa kuizuia. Kwa hiyo Yawe akaniambia: Umwange hasira ile katika barabara juu ya watoto na vilevile juu ya makundi ya vijana; nayo itawaangukia wote, mume na muke, nao wazee na hata wale ambao wamezeeka sana. Nyumba zao zitapewa watu wengine, nayo mashamba yao na wake zao vilevile; maana nitaunyoosha mukono wangu, kuwaazibu wakaaji wa inchi hii. –Ni ujumbe wa Yawe. Wote, tangu mudogo mpaka mukubwa kabisa, kila mumoja anatamani kupata faida isiyokuwa ya haki. Tangu manabii mpaka makuhani, kila mumoja wao ni mudanganyifu. Wanatunza vidonda vya watu wangu juujuu, wakisema: “Kuna amani, kuna amani”, ingawa hakuna amani yoyote! Wao walisikia haya walipofanya machukizo hayo? Hapana! Hawakusikia haya hata kidogo. Hata zamiri hazikuwagonga. Kwa hiyo wataanguka pamoja na wale wanaoanguka; wakati nitakapowaazibu, wataangamizwa kabisa. –Ni Yawe anayesema hivyo. Yawe anasema hivi: Musimame katika masanganjia, muangalie. Muulize juu ya matukio ya zamani. Mutafute pahali panapokuwa njia nzuri muifuate, nanyi mutaweza kupumzika. Lakini wao wakasema: Hatutafuata njia hiyo. Kisha nikawawekea walinzi kwa kuwaarifu nikawaambia: Musikilize mulio wa baragamu. Lakini wao wakasema: Hatutausikiliza. Kwa hiyo, musikilize, enyi mataifa; enyi makundi ya watu, mujue yale yatakayowapata. Sikiliza, ee dunia! Mimi nitawaletea watu hawa hasara kulingana na nia zao mbaya. Maana hawakuyajali maneno yangu, na mafundisho yangu nayo wameyakataa. Kwa nini kuniletea ubani kutoka Seba, na udi wa harufu nzuri kutoka inchi ya mbali? Sadaka zenu za kuteketezwa kwa moto hazikubaliki, wala sadaka zenu zingine hazinipendezi. Kwa hiyo Yawe anasema hivi: Nitawawekea watu hawa vikwazo, ambavyo vitawaangusha chini. Wababa na wana wataangamia, na jirani na rafiki vilevile. Yawe anasema hivi: Muangalie, watu wanakuja toka inchi ya kaskazini; taifa kubwa linajitayarisha kutoka mbali kwa mwisho wa dunia. Wameshika pinde zao na mikuki; ni watu wakali wasiokuwa na huruma. Vishindo vyao ni kama uvumi wa bahari. Wamepanda juu ya farasi, wamejipanga tayari kwa vita na wewe Sayuni! Waisraeli wanasema: Tumesikia habari zao. Kwa hiyo mikono yetu imeregea; tumeshikwa na huzuni na uchungu, kama mwanamuke anayezaa. Hatuwezi kwenda katika mashamba, wala kutembea katika barabara; waadui wameshika silaha katika mikono, vitisho vimejaa kila pahali. Yawe anasema: Muvae magunia, enyi watu wangu na kugaagaa katika majivu. Muomboleze kwa uchungu, kama mutu anayemulilia mwana wake wa pekee, maana mwangamizaji atakuja, na kuwashambulia kwa rafla. Yeremia, wewe nimekuweka kuwa muchunguzi na mupimaji wa watu wangu, kusudi uchunguze na kuzijua njia zao. Wote ni waasi na wagumu, ni watu wanaopitapita wakisengenya wengine, ni wagumu kama shaba au chuma. Wote wanatenda mabaya. Moto wa kufua vyuma unawaka kwa nguvu, risasi inayeyukia humohumo katika moto; ni bure kuendelea kuwatakasa watu wangu, waovu hawawezi kuondolewa uchafu wao. Basi wataitwa “takataka za feza”, maana mimi Yawe nimewakataa. Yawe akamutolea Yeremia ujumbe, akisema: Kwenda kusimama kwenye mulango wa hekalu lake na kutangaza ujumbe huu: Musikilize neno la Yawe enyi watu wa Yuda munaoingia humu kwa kumwabudu Yawe. Yawe wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi: Mugeuze mwenendo wenu na matendo yenu, nami nitawaacha muendelee kukaa pahali hapa. Musitumainie maneno haya ya udanganyifu mukisema: Hili ni hekalu la Yawe, hekalu la Yawe, hakika hili ni hekalu la Yawe. Lakini mugeuze mwenendo wenu na matendo yenu. Mufuate sheria yangu kati yenu. Musiwatese wageni, wayatima au wajane au kuwaua watu wasiokuwa na kosa katika inchi hii. Musijiangamize wenyewe kwa kuabudu miungu mingine. Mukifanya hivyo, mimi nitawaacha mukae siku zote pahali hapa, katika inchi niliyowapa babu wenu tangu zamani. Lakini kumbe, munatumainia maneno ya udanganyifu yasiyokuwa na faida kwenu. Munaiba, munaua, munafanya uzinzi, munaapa kwa uongo, munamufukizia mungu Bali ubani na kuabudu miungu mingine ambayo hamujapata kuijua. Kisha, mutakuja na kusimama mbele yangu katika hekalu hili linalojulikana kwa jina langu na kusema “Tuko salama”, ingawa munaendelea kufanya mambo hayo yanayonichukiza. Munazani kwamba hekalu hili linalojulikana kwa jina langu limekuwa kimbilio la wanyanganyi? Mujue kwamba mimi nimeona yote munayofanya! –Ni ujumbe wa Yawe.– Muende kwenye pahali pangu kule Shilo, nafasi nilipochagua kwa kuabudiwa mara ya kwanza, muone maangamizi niliyofanya kule kwa sababu ya uovu wa watu wangu, Israeli. Ninyi mumefanya mambo hayo yote. –Ni ujumbe wa Yawe.– Na hata niliposema nanyi tena na tena hamukunisikiliza. Nilipowaita hamukuitika. Kwa hiyo, kama vile nilivyoutendea muji wa Shilo, ndivyo nitakavyolitendea hekalu hili linalojulikana kwa jina langu, hekalu ambalo ninyi munalitegemea; ndiyo pahali hapa ambapo niliwapa ninyi na babu zenu. Nitawafukuza ninyi mbali nami kama nilivyowatupilia mbali wandugu zenu, wote wa uzao wa Efuraimu. Nawe Yeremia, usiwaombee watu hawa, usinililie kwa ajili yao, usinililie kwa ajili yao wala kunisihi kwa ajili yao, maana sitakusikiliza. Wewe hauoni mambo wanayofanya katika miji ya Yuda na katika barabara za Yerusalema? Watoto wanaokota kuni, wababa wanawakisha moto na wamama wanaponda unga kwa ajili ya kutengeneza mikate ya kumutambikia mungu wa kike, wanayemwita malkia wa mbinguni. Tena wananikasirikisha kwa kuitolea miungu mingine sadaka ya divai. Lakini ni nani wanayemukasirikisha? Mimi? Hata kidogo! Wanajikasirikisha wao wenyewe na kujifezehesha! –Ni ujumbe wa Yawe. Kwa hiyo, Bwana wetu Yawe anasema hivi: Nitaimwanga hasira yangu juu ya pahali hapa, juu ya wanadamu na nyama, miti katika mashamba na juu ya mazao ya inchi. Nayo nafasi hii itawaka moto wala hautaweza kuzimishwa. Yawe wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi: Muongeze sadaka zenu za kuteketezwa kwa moto juu ya sadaka zenu zingine, nanyi mujikulie nyama zile! Maana, siku nilipowaondoa babu zenu katika inchi ya Misri, sikuwaambia kitu wala kuwapa amri yoyote juu ya sadaka za kuteketezwa na sadaka zingine. Lakini niliwapa amri kwamba waitii sauti yangu kusudi nikuwe Mungu wao, nao wakuwe watu wangu. Niliwaamuru vilevile waishi kama nilivyowaagiza, kusudi wapate uheri. Lakini wao hawakunitii wala kunitegea sikio. Lakini wakafuata mashauri yao wenyewe na ugumu wa mioyo yao, wakarudi nyuma pahali pa kusonga mbele. Tangu siku ile babu zenu walipotoka Misri mpaka leo, sikuchoka kuwatuma kwenu manabii wote, watumishi wangu. Lakini hawakunisikiliza wala kunitegea sikio, lakini wakazidi kufanya vichwa vyao kuwa vigumu na kuasi kuliko hata babu zenu. Sasa wewe Yeremia utawaambia maneno haya yote, lakini wao hawatakusikiliza. Utawaita, lakini hawatakuitikia. Basi utawaambia: Ninyi ni taifa ambalo halikutii sauti ya Yawe, Mungu wao, wala kukubali maonyo yake. Kwenu uaminifu umekufa; umetoweka kabisa katika vinywa vyenu. Munyoe nywele zenu na kuzitupa, enyi wakaaji wa Yerusalema: mufanye maombolezo juu ya vichwa vya milima, maana, mimi Yawe nimewakataa ninyi, nimewatupilia ninyi kizazi kilichosababisha hasira yangu! Watu wa Yuda wametenda maovu mbele yangu. Wameweka sanamu zenye kuchukiza ndani ya nyumba hii inayojulikana kwa jina langu na kuichafua. Wamejenga mazabahu inayoitwa “Tofeti” huko kwenye bonde la Mwana wa Hinomu, kwa kuwatolea wana na wabinti kuwa sadaka ya kuteketezwa kwa moto. Mimi sikukuwa nimewaamuru kufanya jambo hilo, wala halikunifikia katika mafikiri. Kwa sababu hiyo, siku zinakuja ambapo hawataliita tena “Tofeti”, au “bonde la Mwana wa Hinomu”, lakini wataliita “bonde la Mauaji”. –Ni ujumbe wa Yawe.– Huko ndiko watakakozika watu, kwa sababu hapatakuwa pahali pengine pa kuzikia. Maiti za watu hao zitakuwa chakula cha ndege na nyama wa pori, na hapatakuwa mutu atakayewafukuza. Inchi itakuwa jangwa na katika miji ya Yuda na barabara za Yerusalema nitakomesha sauti zote za furaha na shangwe, nazo nyimbo za wenye kufanya ndoa, kwa sababu inchi itakuwa ukiwa. Katika nyakati hizo, mifupa ya wafalme wa Yuda, mifupa ya wakubwa wao, mifupa ya makuhani, mifupa ya manabii na mifupa ya wakaaji wote wa Yerusalema itachimbuliwa toka ndani ya makaburi yao. Itaachwa imetandazwa mbele ya jua na mwezi na nyota zote za mbingu, vitu ambavyo walivyopenda na kuvitumikia, na kuviendea kwa kuuliza shauri na kuviabudu. Mifupa hiyo haitakusanywa wala kuzikwa, lakini itabaki kama vile mboleo juu ya udongo. Watu wote watakaobaki wa jamaa hii mbaya, pahali popote pale nilipowasambaza, wataona heri kufa kuliko kuishi. –Ni ujumbe wa Yawe wa majeshi. Wewe Yeremia utawaambia kwamba: Yawe anasema hivi: Mutu akianguka, hasimami tena? Mutu akipotea, harudii tena katika njia yake? Mbona basi, watu hawa wameacha njia inayokuwa sawa na kuendelea katika upotovu wao? Wanashikamana na miungu yao ya uongo, na kukataa kunirudilia mimi! Mimi nilisikiliza kwa uangalifu, lakini wao hawakusema ukweli wowote. Hakuna mutu anayetubu uovu wake, wala kujiuliza hivi: Nimefanya nini? Kila mumoja wao anashika njia yake, kama farasi anavyokimbia haraka kwa vita. Hata korongo anajua wakati wa kuhama; njiwa, mbaruwayi na koikoi, wanajua nyakati zao za kurudi. Lakini hawa watu wangu hawajui maagizo ya Yawe. Ninyi munajidai kwamba muko na hekima, nanyi munafuata amri zangu mimi Yawe. Lakini kalamu ya uongo ya waandishi imeifanya kuwa uongo. Wenye hekima kati yenu wanafezeheka, watahangaishwa na kunaswa. Wamelikataa neno la Yawe. Basi ni hekima gani wanayokuwa nayo? Kwa hiyo, wake zao nitawatoa kwa waume wengine, nayo mashamba yao nitawapa wengine. Maana, tangu mudogo mpaka mukubwa, kila mumoja ana tamaa ya faida isiyokuwa ya haki. Tangu manabii mpaka makuhani, kila mumoja anatenda kwa udanganyifu. Wanatunza vidonda vya watu wangu juujuu, wakisema: “Kuna amani, kuna amani”, ingawa hakuna amani yoyote! Walisikia haya walipotenda machukizo hayo? Hapana, hawakusikia haya hata kidogo. Hata zamiri hazikuwagonga. Kwa hiyo, wataanguka pamoja na wale walioanguka; nitakapowaazibu, wataangamia. –Ni Yawe anayesema hivyo. Nilitaka kuchuma matunda kutoka kwao. –Ni ujumbe wa Yawe.– Lakini sikupata zabibu hata moja juu ya muzabibu, sikupata tini zozote juu ya muti wa tini; hata majani yao yamekauka. Hata nilichokuwa nimewapa kimetoweka. Watu wanauliza: Kwa nini sisi tunakaa tu hapa? Tukusanyike, tuingie katika miji yenye kuzungukwa na kuta, tuangamie kule! Yawe, Mungu wetu, amekusudia tuangamie, ametupa maji yenye sumu tukunywe, kwa sababu tumemukosea yeye. Tulitazamia kupata amani lakini hakuna kitu kizuri. Tulitazamia kupona lakini tumepatwa na vitisho. Kelele za farasi wa waadui zinasikilika tokea Dani, kwa mulio wa farasi wao wa vita, inchi nzima inatetemeka. Wanafika na kuharibu inchi na vyote vinavyokuwa ndani yake, kuangamiza muji pamoja na wote wanaokaa humo. Basi nitawatumia ninyi nyoka; nyoka wenye sumu wasioweza kulogwa na walozi, nao watawauma ninyi. –Ni ujumbe wa Yawe. Huzuni yangu haiwezi kutulizwa, moyo wangu unaugua ndani yangu. Sikiliza kilio cha watu wangu, kutoka kila upande katika inchi. Yawe hayuko tena katika Sayuni? Mufalme wa Sayuni hayuko tena? Lakini Yawe anasema: Mbona wamenikasirikisha na sanamu zao za kuchongwa, nayo miungu yao ya kigeni? Wakati wa mavuno umepita, nao wakati wa jua kali umekwisha, nasi hatujaokolewa! Mimi ninavunjika moyo, ninaomboleza na kufazaika, kwa sababu watu wangu wameumizwa sana. Hakuna dawa ya kupakaa kule Gileadi? Hakuna muganga kule? Mbona basi watu wangu hawajaponyeshwa? Heri kichwa changu kingekuwa kisima cha maji, na macho yangekuwa chemichemi ya machozi kusudi nipate kulia muchana na usiku, kwa ajili ya watu wangu waliouawa! Heri ningepata kibanda cha wasafiri katika jangwa, ningewaacha watu wangu na kujiendea. Wote ni wazinzi, ni kundi la watu waasi. Ndimi zao ni hatari kama pinde; wameimarika kwa ajili ya uongo na si kwa ajili ya haki. Wanaendelea kutenda uovu kisha uovu, wala hawanitambui mimi. –Ni ujumbe wa Yawe.– Kila mutu ajiepushe na jirani yake, wala asimwaminie ndugu yake! Maana ndugu ni mudanganyifu na kila jirani ni musingiziaji. Kila mutu anadanganya jirani yake, hakuna hata mumoja anayesema ukweli. Wamezifundisha ndimi zao kusema uongo; anatenda uovu kwa kadiri ya kushindwa kabisa kunigeukia. Wanalundika matendo ya kuzulumu juu ya mengine, nao udanganyifu juu ya udanganyifu. Wanakataa kunitambua mimi. –Ni ujumbe wa Yawe.– Kwa hiyo, Yawe wa majeshi anasema hivi: Nitawasafisha na kuwapima kwa moto kama vile chuma. Ni namna gani zaidi ya kuwatendea hawa watu wangu waovu? Ndimi zao ni kama mishale yenye sumu, hawachoki kudanganya; kila mutu anaongea vema na jirani yake, lakini anafanya mipango ya kumushambulia ndani ya moyo wake. Nisiwaazibu kwa sababu ya mambo haya? –Ni ujumbe wa Yawe.– Nisililipize kisasi taifa kama hili? Nitalia na kuomboleza juu ya milima; nitaomboleza juu ya mashamba ya nyama katika jangwa, kwa sababu yamekauka kabisa, hakuna mutu anayepita pahali pale. Hakusikiliki tena sauti za ngombe; ndege na nyama wamekimbia na kutoweka. Yawe anasema: Nitaifanya Yerusalema kuwa mabomoko matupu, nitaifanya kuwa pango la mbweha; na miji ya Yuda nitaifanya kuwa jangwa, pahali pasipokaliwa na mutu yeyote. Nami nikauliza: Kuna mutu anayekuwa na hekima apate kueleza mambo haya? Ni nani aliyeongea na Yawe hata aweze kutangaza kwa nini inchi imeharibiwa na kufanywa tupu kama jangwa hata hakuna mutu anayepita humo? Yawe akajibu na kusema hivi: Ni kwa sababu wamekataa kushika sheria yangu niliyowapa, wamekataa kutii sauti yangu na kufuata mapenzi yangu. Wamefuata ugumu wa mioyo yao, wakaenda kuabudu miungu inayoitwa Mabali kama walivyofundishwa na babu zao. Basi, Yawe wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi: Nitawakulisha watu hawa uchungu na kuwapa maji yenye sumu wakunywe. Nitawatawanya kati ya mataifa ambayo wao wenyewe wala babu zao hawakupata kuyajua; na kisha nitatuma vita nyuma yao mpaka hapo nitakapowaangamiza wote. Yawe wa majeshi anasema hivi: Mufikiri na kuwaita wanawake waombolezaji; muwaite wanawake wanaoelewa nyimbo za kilio. Muwaambie hivi: Mukuje upesi muomboleze juu yetu, macho yetu yapate kutiririka machozi, na kope zetu zibubujike machozi kama maji. Kilio hiki kinasikilika Sayuni: Tumeangamia kabisa! Tumefezeheshwa kabisa, kwa maana sherti tuiache inchi yetu, nazo nyumba zetu zibomolewe! Enyi wanawake, musikilize neno la Yawe! Mutege masikio musikie jambo analosema. Muwafundishe wabinti zenu kuomboleza, na kila mutu amufundishe jirani yake wimbo huu wa maziko: Kifo kimetuingilia katika madirisha yetu, kimetupangia katika nyumba zetu nzuri; kimewaangukia watoto wetu katika barabara, nao vijana wetu katika viwanja vya makutano. Sema: Huu ni ujumbe wa Yawe: Maiti za watu zinalala chini kila pahali kama malundo ya mboleo katika mashamba, kama miganda iliyoachwa na muvunaji, wala hakuna anayeikusanya. Yawe anasema hivi: Mwenye hekima asijivunie hekima yake, mwenye nguvu asijivunie nguvu yake; wala tajiri asijivunie utajiri wake. Anayetaka kujivuna, ajivune kwamba ananifahamu mimi, kwamba anajua kwamba mimi Yawe ninatenda mema, ninafanya mambo ya haki kufuatana na sheria yangu katika dunia. Watu wa namna hiyo ndio wanaonipendeza. –Ni ujumbe wa Yawe. Siku zinakuja ambapo nitawaazibu wote waliotahiriwa kimwili tu. –Ni ujumbe wa Yawe.– Ni kusema nitawaazibu: Wamisri, Wayuda, Waedomu, Waamoni, Wamoabu na wakaaji wote wa jangwa wanaonyoa nywele zote za pembenipembeni ya kichwa. Maana watu hawa wote na Waisraeli wote hawajatahiriwa mioyo yao. Enyi Waisraeli musikilize neno Yawe analowaambia. Yawe anasema hivi: Musiige mwenendo wa mataifa mengine, wala musishangazwe na vitambulisho vya ajabu munavyoviona katika mbingu; muyaache mataifa mengine yashangazwe navyo. Maana, desturi za dini za watu hao ni za uongo. Kwa maana mutu anakata muti katika pori, naye fundi anachonga sanamu ya mungu kwa shoka. Kisha watu wanaipamba kwa feza na zahabu wakiipigilia misumari na nyundo kusudi isianguke. Sanamu zao ni kama sanamu za kutishia ndege katika shamba la maboga, hazina uwezo wa kuongea; ni lazima zibebwe maana haziwezi kutembea. Musiziogope sanamu hizo, maana haziwezi kuzuru, wala haziwezi kutenda jambo lolote jema. Ee Yawe, hakuna anayekuwa kama wewe; wewe ni mukubwa na nguvu yako inajulikana. Nani asiyekuogopa wewe, ee mufalme wa mataifa? Wewe unastahili kuheshimiwa: kwa maana kati ya wenye hekima wote wa mataifa, na katika falme zao zote, hakuna hata mumoja anayekuwa kama wewe. Wote ni wajinga na wapumbafu, fundisho la sanamu hizi ni mazarau matupu! Sanamu hizo zinapambwa kwa feza kutoka Tarsisi, na zahabu kutoka Ofiri; zilitengenezwa na wafundi na wafua zahabu. Zimevalishwa nguo nzuri za rangi ya samawi na nyekundu-nyeusi, zilizofumwa na wafundi wa kufuma. Lakini Yawe ni Mungu wa kweli, Mungu Mwenye Uzima, mufalme wa milele. Akikasirika, dunia inatetemeka, mataifa hayawezi kuvumilia hasira yake. Basi, utawaambia hivi: Miungu hiyo ambayo haikuumba mbingu na dunia itaangamia. Itatoweka kabisa toka katika dunia, hapa chini ya mbingu. Yawe aliiumba dunia kwa nguvu zake; kwa hekima yake alisimamisha ulimwengu imara, kwa akili yake alizitandika mbingu juu. Anapotoa sauti, maji yananguruma katika mbingu, anapandisha mawingu toka kwa miisho ya dunia. Anaufanya umeme upige wakati wa mvua, na kuuvumisha upepo katika gala zake. Mwanadamu ni mujinga na mupumbafu; kila mufua zahabu anafezeheshwa na sanamu zake. Sanamu hizo ni uongo mutupu, hazina uzima wowote ndani yao. Hazina faida, ni udanganyifu mutupu; wakati zitakapoazibiwa zote zitaangamia. Lakini Mungu wa Yakobo si kama sanamu hizo, maana, yeye ndiye aliyeumba vitu vyote, na Israeli ni taifa linalokuwa mali yake; Yawe wa majeshi, ndilo jina lake. Mufunge vitu vyenu, enyi watu muliozungukwa kwa vita. Maana Yawe anasema hivi: Mara hii nitawatupa inje wakaaji wa inchi hii, nitawataabisha hata kusibaki mutu yeyote. Ole wangu mimi Yerusalema, maana nimeumizwa sana! Kidonda changu ni kikubwa sana! Mimi nilikuwa nikijisemesha hivi: Hakika haya ni magumu tu, nami ninapaswa kuyavumilia. Lakini hema yangu imebomolewa, kamba zake zote zimekatika; watoto wangu wameniacha, na kujiendea, wala hawako tena; hakuna wa kunisimikia tena hema yangu, wala wa kunitundikia mapazia yangu. Nami Yeremia nikasema: Wachungaji wamekuwa wajinga, hawakuuliza shauri kwa Yawe; kwa sababu hiyo, hawakufanikiwa, na kondoo wao wote wamesambaa. Musikilize ile fujo! Angalia inakuja. Kunatokea shindo kubwa upande wa kaskazini. Taifa kutoka kaskazini linakuja kuifanya miji ya Yuda kuwa jangwa, wataigeuza mapango ya mbweha! Ninajua, ee Yawe, mwanadamu hana uwezo juu ya maisha yake; hakuna mutu anayeweza kuongoza maisha yake. Utuonye, ee Yawe, lakini si kwa kasirani, wala kwa hasira yako, kusudi tusiangamie. Umwange hasira yako juu ya mataifa yasiyokuabudu, na juu ya watu ambao hawakutambui. Maana, wamewaua wazao wa Yakobo; wamewaua na kuwaangamiza kabisa, na inchi yao wameiacha mabomoko. Yawe akanitolea mimi Yeremia ujumbe, akisema: Sikiliza maneno ya agano hili, kisha uende kuyatangazia watu wa Yuda na wakaaji wa Yerusalema. Utawaambia hivi: Yawe, Mungu wa Israeli, anasema hivi: Alaaniwe mutu yeyote asiyeshika masharti ya agano hili. Hili ni agano nililowaagiza babu zenu kutii nilipowaondoa katika inchi ya Misri, kutoka katika shimo la moto. Niliwaambia wanitii na kufanya yote niliyowaamuru, na kwamba wakifanya hivyo, watakuwa watu wangu, nami nitakuwa Mungu wao. Na kwa njia hiyo mimi nitatimiza ahadi niliyowatolea babu zenu, kwamba nitawapa inchi inayojaa maziwa na asali, kama inavyokuwa hata leo. Nami nikajibu: Ikuwe hivyo, ee Yawe. Yawe akaniambia: Tangaza maneno hayo yote katika miji ya Yuda na katika barabara za Yerusalema. Uwaambie watu wayasikilize masharti ya agano hili na kuyashika. Maana niliwaonya vikali babu zao nilipowaondoa katika inchi ya Misri, nami nimeendelea kuwaonya wanitii mpaka siku hii ya leo. Lakini wao hawakunitii, wala hawakunisikiliza. Kila mumoja wao alizidi kuwa mugumu na mwovu. Basi, niliwaazibu kulingana na masharti ya agano hili nililowaamuru kushika, lakini hao wakakataa kulishika. Tena Yawe akaniambia: Watu wa Yuda na wakaaji wa Yerusalema wanafanya shauri baya la kuniasi. Wameurudilia uovu wa babu zao ambao walikataa kusikiliza maneno yangu; wanaiabudu miungu mingine na kuitumikia. Watu wa Israeli na watu wa Yuda wamevunja agano nililofanya na babu zao. Kwa hiyo, Yawe anasema hivi: Nitaleta hasara juu yao ambayo hawataweza kuiepuka. Hata kama wakinililia namna gani, sitawasikiliza. Kwa hiyo wakaaji wa Yuda na wa Yerusalema watakapoiendea miungu yao ambayo wanaifukizia ubani, lakini miungu hiyo haitaweza kuwaokoa wakati huo wa hasara itakayowapata. Enyi watu wa Yuda, hesabu ya miji yenu ni sawasawa na hesabu ya miungu yenu. Na kama vile barabara zenu za Yerusalema zinavyokuwa nyingi, ndivyo mulivyojenga mazabahu ya haya, ni kusema ya kufukizia ubani kwa mungu Bali. Basi, wewe Yeremia, usiwaombee watu hawa, usinililie kwa ajili yao, wala kunisihi. Maana, hata wakiniomba watakapokuwa katika hasara, sitawasikiliza. Yawe anasema: Watu wangu wapendwa wana haki gani ya kuingia ndani ya hekalu langu ikiwa wametenda maovu? Wanazani kwamba viapo vyao na sadaka zao wanazonitolea zitawakingia hasara ile. Wakati fulani, mimi nilisema kwamba wao ni muzeituni wenye majani mabichi, muzeituni muzuri na wenye matunda mema; lakini sasa, kwa ngurumo ya zoruba kubwa, nitauchoma kwa moto na kuyateketeza matawi yake. Mimi Yawe wa majeshi niliuotesha huu muzeituni; lakini sasa ninatangaza hasara juu yake, kwa sababu ya maovu ambayo watu wa Israeli na Yuda wameyafanya. Wamenikasirikisha kwa kumufukizia mungu Bali ubani. Yawe alinijulisha, nami nikaelewa; Yawe alinijulisha shauri lao baya. Nami nilikuwa kama kondoo mupole anayepelekwa kuchinjwa; sikujua kwamba shauri walilofanya lilikuwa juu yangu. Wao walisema: Tuuharibu muti pamoja na matunda yake, tumwue apate kusahaulika katika dunia, jina lake lisikumbukwe tena. Lakini, ee Yawe wa majeshi, wewe unayehukumu kwa haki, unayechunguza mioyo na akili za watu, unijalie nione jinsi utakavyowalipiza kisasi, maana ninayaweka maneno yangu kwako. Kwa hiyo Yawe wa majeshi anasema hivi juu ya watu wa Anatoti ambao wanataka kuniua na kuniambia: Usitutabirie kwa jina la Yawe, kama si vile tutakuua. Ndiyo, Yawe wa majeshi anasema hivi: Nitawaazibu watu hao. Vijana wao watauawa kwa upanga; watoto wao wanaume na wanawake watakufa kwa njaa. Nimepanga muda wa kuleta maangamizi juu ya watu wa Anatoti. Wakati huo utakapofika, hakuna hata mumoja wao atakayebaki muzima. Ee Yawe, wewe ni mwenye haki, ingawa nitakushitaki. Lakini ningependa nibishane nawe juu ya mambo ya haki: Kwa nini waovu wanafanikiwa katika mambo yao? Mbona wote wanaodanganya wanastawi? Umewapanda nao wameota mizizi, wanastawi na kuzaa matunda. Wanakujua kwa midomo tu, lakini mioyo yao iko mbali nawe. Lakini wewe ee Yawe unanijua; umeniona na kunipima. Unajua namna ninavyokutegemea, uwatayarishe kwa ajili ya siku ya kuuawa. Mpaka wakati gani inchi itaomboleza kwa kukauka, na nyasi za mashamba yote kunyauka? Nyama na ndege wanakufa kwa uovu wa wakaaji wake. Wao wanasema: Mungu hataona mwisho wetu. Yawe akaniambia: Ikiwa umekimbia pamoja na wenye kukimbia kwa miguu, nao wamekuchokesha, basi, namna gani utaweza kushindana na farasi? Kama unaanguka katika inchi isiyokuwa na vizuizi, utafanya nini katika pori la Yordani? Hata wandugu zako, jamaa yako mwenyewe, nao vilevile wanakudaganya; wanakukaripia waziwazi. Usiwaamini hata kidogo, ingawa wanakuambia maneno mazuri. Yawe anasema hivi: Nimeiacha nyumba yangu; nimeitupa mali yangu mimi mwenyewe. Israeli, mupenzi wangu wa moyo, nimemutoa katika mikono ya waadui zake. Wachaguliwa wangu wamenigeuka, wamekuwa kama simba katika pori, wameningurumia mimi; ndiyo maana ninawachukia. Urizi wangu umekuwa kama ndege muzuri ambaye anashambuliwa pande zote na ndege wakali? Muende kuwakusanya nyama wote wa pori, muwalete wakule. Wachungaji wengi wameharibu shamba langu la mizabibu, wamekanyagakanyaga chini urizi wangu; shamba langu zuri wamelifanya jangwa. Wamelifanya kuwa tupu; nalo linalilia katika ukiwa wake. Inchi yote imekuwa jangwa, wala hakuna mutu anayejali. Waangamizaji wamefika, tokea juu ya milima yote katika jangwa. Upanga wangu unapita kuiangamiza inchi, toka upande mumoja mpaka mwingine, wala hakuna mutu atakayeishi kwa amani. Walipanda ngano, lakini walivuna magugu; wamejichokesha kwa bure. Kwa sababu ya hasira kali ya Yawe, watasikia haya juu ya mavuno yao. Yawe anasema hivi juu ya jirani wabaya za watu wake: Wamegusa sehemu ya urizi wangu, niliowapatia watu wangu Waisraeli! Basi nitawaongoa kutoka katika inchi yao, na hata watu wa Yuda nitawaongoa katika inchi yao. Lakini kisha kuwaongoa, nitawahurumia tena; nitalirudisha kila taifa katika sehemu yake na katika inchi yake. Na kama watajifunza mwenendo wa watu wangu kwa moyo wote, wakiapa kwa jina langu, wakisema “Kama vile Yawe anavyoishi”, kama vile walivyowafundisha watu wangu kuapa kwa jina la mungu Bali, basi watastawi katikati ya watu wangu. Lakini taifa lolote ambalo halitanitii, nitaliongoa kabisa na kuliangamiza. –Ni ujumbe wa Yawe. Yawe aliniambia hivi: Kwenda ununue mukaba na kuuvaa katika kiuno; lakini usiutie ndani ya maji. Basi, nikaenda, nikanunua mukaba kama vile Yawe alivyoniagiza, nami nikauvaa katika kiuno. Kisha, neno la Yawe lilinifikia kwa mara ya pili kusema hivi: Twaa ule mukaba ulioununua na ambao unaouvaa katika kiuno, uende kwenye muto Furati na kuuficha katika pango chini ya jiwe. Basi, nikaenda na kuficha ule mukaba karibu na muto Furati, kama vile Yawe alivyoniamuru. Kulipokwisha kupita siku nyingi, Yawe akaniambia: Kwenda kwenye muto Furati, utwae ule mukaba niliokuamuru kuuficha huko. Basi, nikaenda kwenye muto Furati, nikachimbua na kuuondoa ule mukaba pahali nilipokuwa nimeuficha. Nilipouondoa, niliona kwamba ulikuwa umeharibika kabisa; nao ulikuwa haufai tena. Neno la Yawe lilinifikia kusema hivi: Yawe anasema hivi: Hivi ndivyo nitakavyokiharibu kiburi cha watu Yuda na kiburi kikubwa cha watu wa Yerusalema. Watu hawa waovu wanakataa kusikia maneno yangu. Wanaendelea na kufuata mawazo yao wenyewe. Wanaifuata miungu mingine, wanaitumikia na kuiabudu. Hao watakuwa kama mukaba huu ambao haufai kitu. Kama vile mukaba unavyoshikamana na kiuno cha mutu, ndivyo nilivyowashikamanisha nami watu wa Israeli na watu wa Yuda, kusudi wajulikane kwa jina langu, wanisifu na kunitukuza. Lakini wao hawakunisikiliza. –Ni ujumbe wa Yawe. Uwaambie watu wa Yuda hivi: Yawe, Mungu wa Israeli, anasema hivi: Kila mutungi utajazwa divai. Utakapowaambia hivyo, wao watakujibu hivi: Unazani sisi hatujui kwamba kila mutungi utajazwa divai? Nawe utawajibia hivi: Yawe anasema hivi: Nitawalewesha wakaaji wote wa inchi hii; wafalme wanaotawala kwa kiti cha kifalme cha Daudi, makuhani, manabii na wakaaji wote wa Yerusalema. Nitawagonganisha wao kwa wao hata baba na watoto. –Ni ujumbe wa Yawe.– Sitawahurumia, sitawaachilia wala sitawarehemu, mpaka nitakapowaangamiza. Enyi Waisraeli, musikilize kwa uangalifu, musikuwe na kiburi maana Yawe anasema nanyi. Mumutukuze Yawe, Mungu wenu, mbele hajawaletea giza, mbele hamujajikwaa miguu kwenye milima inayofunikwa na giza. Ninyi mulitazamia mwangaza, lakini anaugeuza kuwa usiku anaufanya kuwa giza nzito. Na kama musiponisikiliza, moyo wangu utalia machozi kwenye uficho, kwa sababu ya kiburi chenu. Nitalia kwa uchungu na kutoa machozi, maana watu wa Yawe wanapelekwa katika uhamisho. Muambie mufalme na malkia mama yake hivi: Mushuke toka kwenye viti vyenu vya kifalme, maana taji zenu nzuri zimeanguka toka juu ya vichwa vyenu. Miji ya Negebu imezungukwa kwa vita; hakuna anayeweza kuingia ndani yao. Watu wa Yuda wamekamatwa mateka, wote kabisa wamepelekwa katika utumwa. Inua macho yako, ee Yerusalema! Angalia! Waadui zako wanakuja kutoka kaskazini. Kundi ulilopewa liko wapi? Kundi lako zuri liko wapi? Utasema nini juu ya wale uliowazoeza kuwa warafiki zako, wale ambao wewe mwenyewe uliwafundisha, watakapokushinda na kukutawala? Si utashikwa na uchungu sawa vile mwanamuke anayezaa? Nawe utajiuliza hivi katika moyo wako: Kwa nini mambo haya yamenipata? Sawa! Ikiwa kanzu yako imepandishwa, na kutendewa kwa kinguvu, hayo ni matokeo ya makosa yako mengi sana. Mwetiopia anaweza kubadilisha rangi yake, au chui madoadoa yake? Nanyi muliozoea kufanya mabaya, munaweza namna gani kutenda mema? Yawe atawasambaza kama maganda yanayopeperushwa na upepo unaovuma kutoka katika jangwa. Yawe anasema: Hayo ndiyo yatakayokupata, ni hivi nilivyoamua kukutendea, kwa sababu umenisahau mimi na kutegemea miungu ya uongo. –Ni ujumbe wa Yawe.– Nitapandisha kanzu yako mpaka kwenye kichwa hata uchi wako upate kuonekana wazi. Nimeyaona machukizo yako: nimeona uzinzi wako na utongozaji wako, na uasherati wako usiousikilia haya, unaoufanya juu ya milima na katika mashamba. Ole kwako wewe Yerusalema! Mpaka wakati gani utabaki bila kutakaswa? Yawe akanitolea mimi Yeremia ujumbe juu ya ule ukosefu wa maji, akisema: Watu wa Yuda wanaomboleza, miji yake inateketea. Watu wake wanaomboleza wakiikaa katika udongo na kilio cha Yerusalema kinapanda mpaka juu. Wakubwa wake wanawatuma watumishi wao maji; watumishi wanakwenda kwenye visima, lakini hawapati maji; wanarudi na vyombo vitupu. Kwa ajili ya haya na mahangaiko wanaangalia chini. Walimaji wanahuzunika kwa kuona jinsi udongo unavyokauka kwa ajili ya ukosefu wa mvua. Hata kulungu anazaa katika pori na kuacha kitoto chake, kwa sababu hakuna majani. Punda wa pori wanasimama kwenye vichwa vya vilima vyenye kukauka, wakivuta hewa kama mbweha; macho yao yanafifia kwa ukosefu wa majani. Nao watu wanasema: Ingawa zambi zetu zinatoa ushuhuda juu yetu, utusaidie ee Yawe kwa ajili ya heshima ya jina lako. Maasi yetu ni mengi, tumetenda zambi mbele yako. Wewe unayekuwa tumaini la Waisraeli, wewe unayetuokoa wakati wa taabu, namna gani unajifanya kama mugeni katika inchi, kama musafiri anayelala kwa usiku mumoja tu? Namna gani unakuwa kama mutu aliyechanganyikiwa, kama shujaa asiyeweza kusaidia mutu? Ingawa hivyo wewe ee Yawe unakaa katikati yetu; nasi tunajulikana kwa jina lako, usituache. Yawe anasema hivi juu ya watu hawa: Kweli wamependa sana kutangatanga, wala hawakujizuia; kwa hiyo mimi Yawe sipendezwi nao. Sasa nitayakumbuka makosa yao, na kuwaazibu kwa ajili ya zambi zao. Yawe akaniambia hivi: Usiwaombee watu hawa uheri. Hata wakifunga, sitayasikiliza maombi yao, na hata wakinitolea sadaka za kuteketeza kwa moto na sadaka zingine, mimi sitazikubali. Lakini nitawaangamiza kwa vita, njaa na ugonjwa mukali. Kisha mimi nikasema: Ee Bwana wangu Yawe! Manabii wanawaambia watu hawa kwamba hakutakuwa vita wala njaa, kwa sababu umeahidi kwamba kutakuwa tu amani katika inchi hii. Naye Yawe akaniambia: Hao manabii wanatoa unabii wa uongo kwa jina langu. Mimi sikuwatuma, wala sikuwaamuru, wala sikusema nao. Wanawatabiria maono ya uongo, maaguzi yao hayana maana yoyote, wao wanajitungia uongo wenyewe. Kwa hiyo, Yawe anasema hivi juu ya hao manabii: Wanatabiri kwa jina langu, ingawa mimi sikuwatuma. Wanasema kwamba hakutakuwa vita wala njaa katika inchi hii: Manabii hao wataangamia kwa vita na kwa njaa. Na hao ambao waliowatabiria mambo hayo, maiti zao zitatupwa katika barabara za Yerusalema wakiuawa kwa njaa na vita, wala hakutakuwa mutu wa kuwazika wao wenyewe, wake zao, wabinti zao na wana wao. Mimi nitawabebesha lazima ya uovu wao wenyewe. Hivi ndivyo utakavyowaambia: Heri macho yangetoa machozi usiku na muchana, wala yasikome kutiririka, maana, watu wangu wamepata hasara kubwa, wameumizwa kidonda kikubwa sana. Nikienda inje katika mbuga, ninaiona maiti ya waliouawa kwa vita; nikiingia ndani katika muji, ninaona tu maiti ya waliokufa kwa njaa! Manabii na makuhani wanashugulikia mambo yao katika inchi, lakini hawajui wanalofanya. Ee Yawe, umekataa Yuda kabisa? Moyo wako umechukizwa na Sayuni? Kwa nini umetupiga vibaya kama hivi, hata hatuwezi kupona tena? Tulitazamia kupata amani, lakini hakuna kitu kizuri. Tulitazamia kupona, lakini tumepatwa na vitisho. Tunakubali uovu wetu, ee Yawe, tunakubali uovu wa babu zetu, maana, tumekukosea wewe. Usitutupe, kwa ajili ya heshima ya jina lako; usikizarau kiti chako cha kifalme chenye utukufu. Ukumbuke agano ulilofanya nasi, wala usilivunje. Katikati ya miungu ya uongo ya mataifa nani anayeweza kunyesha mvua? Au, ni mbingu ndiyo inaweza kutoa manyunyu? Si ni wewe ee Yawe, Mungu wetu? Tunakuwekea wewe tumaini letu, maana ni wewe unayefanya haya yote. Kisha Yawe akaniambia: Hata kama Musa na Samweli wangesimama mbele yangu na kunisihi, singewahurumia watu hawa. Uwaondoe kabisa mbele yangu. Uwaache waende! Na kama wakikuuliza: Tutaenda wapi? Wewe utawajibu kwamba: Yawe anasema hivi: Walioandikiwa kufa kwa ugonjwa mukali, watakufa kwa ugonjwa mukali, walioandikiwa kufa kwa vita, watakufa kwa vita, walioandikwa kufa kwa njaa, watakufa kwa njaa; nao walioandikiwa kupelekwa katika utumwa, watapelekwa katika utumwa. Nimeamua kuleta aina ine za maangamizi juu yao: upanga kwa kuwaua, imbwa kwa kuwararua, ndege na nyama wa pori kwa kuwakula na kuwamaliza. Nitawafanya kuwa kitu cha kutisha kwa falme zote za dunia, kwa sababu ya mambo ambayo Manase mwana wa Hezekia, aliyofanya kule Yerusalema, alipokuwa mufalme wa Yuda. –Ni ujumbe wa Yawe. Ni nani atakayewahurumia, enyi watu wa Yerusalema? Ni nani atakayeomboleza juu yenu? Nani atasimama kuuliza habari zenu? Ninyi mumenikataa mimi. –Ni ujumbe wa Yawe.– Ninyi mumeniacha na kurudi nyuma. Kwa hiyo nimenyoosha mukono kwa kuwaangamiza. Nimechoka na kuwahurumia. Nimepepeta watu wangu kwa kuwasambaza sawa maganda, toka katika kila muji wa inchi yao. Nimewaangamiza kwa kuwaua watoto wao, lakini hawakuacha mwenendo wao. Wajane wao wamekuwa wengi kuliko muchanga wa bahari. Nao wamama wenye watoto vijana nimewaletea mwangamizaji muchana kati. Nimesababisha uchungu na vitisho viwapate kwa rafla. Mama aliyeheshimiwa kwa kuwa na watoto saba, sasa kwa rafla hana kitu. Amezimia na kukata roho, amekufa angali kijana, amefezeheka na kuzarauliwa. Na wale watakaobaki wazima nitawatoa kwa upanga mbele ya waadui zao. –Ni ujumbe wa Yawe. Ole wangu, mama yangu, kwa sababu ulinizaa! Mimi nimekuwa mutu wa ubishi na ugomvi katika inchi yote! Sijapata kukopesha mutu wala kukopeshwa na mutu, lakini kila mutu ananilaani. Basi, ee Yawe, acha laana hizo zinipate kama sikukutumikia vizuri na kama sikukusihi kwa ajili ya waadui zangu wakati walipokuwa katika taabu na shida! Mutu anaweza kuvunja chuma, kile chuma au shaba inayotoka kaskazini? Yawe anasema: Nitazifanya mali zenu na akiba zenu zitekwe tena, wala hamutapewa malipo yoyote ya vitu hivyo kwa sababu ya zambi zenu zote mulizozitenda kila pahali katika inchi. Nitawafanya muwatumikie waadui zenu katika inchi musiyoijua kwa sababu hasira yangu imewaka kama moto usiozimika hata milele. Nami nikasema: Lakini wewe Yawe unanielewa vizuri; unikumbuke na kuja kunisaidia. Unilipizie watesaji wangu kisasi. Wewe ni muvumilivu, usiniache niangamie; kumbuka kwamba ninatukaniwa kwa ajili yako. Palepale maneno yako yaliponifikia, niliyameza; nayo yakanifurahisha, yakakuwa matamu katika moyo wangu, maana mimi ninajulikana kwa jina lako, ee Yawe wa majeshi. Mimi sikuikaa pamoja na wanaojifurahisha, wala sikufurahi pamoja nao. Niliikaa peke yangu nikilemewa na nguvu yako; kwa maana ulinijaza hasira yako. Kwa nini mateso yangu hayaishi? Mbona kidonda changu hakiponi nacho hakitaki kutunzwa? Kama vile kijito chenye kukaukakauka, kisivyoweza kutumainiwa, ndivyo wewe umekuwa kwangu! Basi, Yawe akasema hivi: Kama ukinirudilia, nitakurudisha katika hali yako ya mbele, nawe utanitumikia tena. Kama ukisema maneno ya maana, yasiyokuwa ya upuuzi, basi utakuwa musemaji wangu. Watu watakufikia wewe, wala si wewe utakayehitaji kuwaendea. Mbele ya watu hawa, nitakufanya sawa ukuta mugumu wa shaba. Watapigana nawe, lakini hawataweza kukushinda, maana, mimi niko pamoja nawe, nipate kukuokoa na kukukomboa. –Ni ujumbe wa Yawe.– Nitakuokoa toka katika mikono ya watu waovu, na kukuopoa toka katika makucha ya watesaji. Neno la Yawe lilinifikia kusema hivi: Wewe usioe wala kuzaa watoto pahali hapa. Maana Yawe anasema hivi juu ya wana na wabinti watakaozaliwa pahali hapa na juu ya wazazi wao: Hao watakufa kwa magonjwa makali, na hakuna atakayeomboleza juu yao wala kuwazika. Maiti zao zitabaki kama vile mboleo juu ya udongo. Wataangamia kwa vita na kwa njaa; na maiti zao zitakuwa chakula cha ndege na nyama wa pori. Yawe anasema hivi: Usiingie katika nyumba yenye kilio wala usiende kuomboleza wala kuwalilia. Kwa maana sitawapatia watu hawa amani tena. Sitawatendea tena mema wala kuwasikilia huruma. –Ni ujumbe wa Yawe.– Wote, wakubwa kama vile wadogo, watakufa katika inchi hii; nao hawatazikwa, wala hakuna atakayeomboleza juu yao. Hakuna atakayejikatakata wala kunyolewa upaa kwa ajili ya kifo chao. Hakuna atakayechangia chakula na yule aliyekufiwa kwa kumufariji, wala kumupatia kinywaji cha kumufariji kwa ajili ya kukufiwa na mama au baba yake. Usiingie katika nyumba watu wanamofanya karamu. Usiikae kula na kunywa pamoja nao. Maana Yawe wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi: Nitazikomesha kabisa kutoka pahali hapa sauti za furaha na shangwe, nazo nyimbo za wenye kufanya ndoa. Nitayafanya hayo yote katika nyakati zenu, na mutayaona waziwazi. Nawe utakapowaambia watu hao maneno haya yote, wao watakuuliza: Kwa nini Yawe amekusudia hasara hii kubwa juu yetu? Tumefanya uovu gani? Tumetenda zambi gani mbele ya Yawe, Mungu wetu? Nawe utawajibu hivi: Babu zenu waliniacha. Wakafuata miungu mingine, wakaitumikia na kuiabudu. Waliniacha, wala hawakuzitii sheria zangu. Ninyi mumefanya vibaya zaidi kuliko babu zenu, maana kila mumoja wenu ni mwenye moyo mugumu na mwenye nia mbaya, wala hamunisikilizi. Kwa hiyo, nitawafukuza toka katika inchi hii na kuwapeleka mpaka kwenye inchi ambayo ninyi wenyewe wala babu zenu hawakuijua. Kule mutaitumikia miungu mingine usiku na muchana, wala sitawasikilia ninyi huruma. –Ni ujumbe wa Yawe. Kwa hiyo, siku zinakuja ambapo watu hawataapa tena wakisema: Kama vile Yawe anavyoishi, yule aliyewaondoa Waisraeli kutoka inchi Misri. Lakini wataapa wakisema: Kama vile Yawe anavyoishi, yule aliyewaondoa Waisraeli kutoka katika inchi ya kaskazini na kutoka katika inchi zote ambapo alipowasambaza. Maana, nitawarudisha katika inchi yao niliyowapatia babu zao. –Ni ujumbe wa Yawe. Nitaita wavuvi wengi kuja kuwanasa watu hawa. Kisha, nitaita wawindaji wengi kuja kuwawinda juu ya kila mulima, kila kilima na katika mapango ya chini ya mawe. Maana, mimi ninayaona matendo yao yote, hakuna hata moja linalofichama mbele yangu. Maovu yao yote ni wazi mbele yangu. Nitalipiza kisasi mara mbili zaidi juu ya zambi zao na makosa yao, kwa sababu wameichafua inchi yangu na mizoga ya miungu yao yenye kuchukiza, wameijaza inchi yangu na hayo machukizo yao. –Ni ujumbe wa Yawe. Ee Yawe! Wewe ndiwe nguvu yangu na upango wangu; wewe ni kimbilio langu wakati wa taabu. Mataifa toka pande zote za dunia yatakufikia na kusema: Miungu ya babu zetu ilikuwa ya uongo, ilikuwa ya bure, isiyofaa kitu. Mwanadamu anaweza kujitengenezea miungu? Kweli hiyo si miungu hata kidogo! Kwa hiyo, Yawe anasema: Wakati huu nitawafundisha kusudi wapate kutambua waziwazi nguvu zangu na uwezo wangu, nao watajua kwamba jina langu ni Yawe. Zambi ya watu wa Yuda, haiwezi kufutikana, imeandikwa kwa kalamu ya chuma; kwa chongo ya almasi. Imechorwa ndani ya mioyo yao na kwenye pembe za mazabahu yao. Watoto wao wanakumbuka mazabahu zao na sanamu za mungu muke, Ashera, zilizowekwa kando ya miti mibichi, juu ya vilele vya vilima na juu ya milima katika mbuga. Mali yenu na akiba zenu zote nitazitoa zitekwe kwa kulipia zambi zenu mulizotenda kila pahali katika inchi yenu. Itawabidi kuiacha hiyo inchi yenu niliyowapa, nami nitawafanya muwatumikie waadui zenu katika inchi musiyoijua, kwa sababu hasira yangu imewaka kama moto usiozimika hata milele. Yawe anasema hivi: Alaaniwe mutu anayemutegemea mwanadamu, mutu ambaye anategemea nguvu za mwanadamu, mutu ambaye moyo wake umegeuka mbali nami Yawe. Huyo ni kama kichaka katika jangwa, hataona mazuri yoyote. Ataishi pahali penye kukauka katika jangwa, kwenye udongo ulioharibiwa na chumvi, na usiokaliwa na watu. Abarikiwe mutu anayenitegemea mimi Yawe, mutu ambaye mimi Yawe ndiye tegemeo lake. Huyo ni kama muti uliopandwa kando ya maji, unaopenyeza mizizi yake karibu na chemichemi. Hauogopi wakati wa jua kali, majani yake yanabaki mabichi. Hauhangaiki katika mwaka wa ukosefu wa mvua, nao haukosi kuzaa matunda. Moyo wa mutu ni mudanganyifu kuliko vitu vyote; hauwezi kuponyeshwa, hakuna anayeweza kuuelewa! Mimi Yawe ninapima akili na kuchunguza moyo wa mutu. Na hivyo ninamutendea kila mumoja, kulingana na mwenendo wake, kadiri ya matendo yake. Mutu anayepata mali isiyokuwa ya usawa ni kama kwale anayelalia mayai ambayo hakutaga. Mali yanamwishia angali kijana, na kwa mwisho anageuka sawa mupumbafu. Kuna kiti cha kifalme chenye utukufu kinachoinuka juu tangu mwanzo wa vyote, ndipo pahali petu patakatifu. Ee Yawe, tumaini la Waisraeli, wote wanaokukataa wafezeheshwe. Wanaokuacha wewe watatoweka, kama majina yaliyoandikwa chini katika mavumbi, kwa maana wamekuacha wewe Yawe, unayekuwa chemichemi ya maji ya uzima. Uniponyeshe, ee Yawe, nami nitapona; uniokoe, nami nitaokoka; maana, wewe ndiwe sifa yangu. Angalia jinsi watu wanavyoniambia: Vile vitisho vya Yawe viko wapi? Vifike basi! Sikukukaza kutenda mabaya, wala sikutamani ile siku ya hasara ifike. Wewe mwenyewe unajua maneno niliyosema mbele yako. Usiniletee hofu; maana wewe ndiwe kimbilio langu siku ya hasara. Uwapatishe haya wale wanaonitesa, lakini usiniache mimi kupata haya. Uwafezeheshe watu hao, lakini usiniache mimi kufezeheka. Uwaletee ile siku ya hasara, uwaangamize kabisakabisa! Yawe aliniambia hivi: Kwenda usimame kwenye Mulango wa Wanainchi, ambako wafalme wa Yuda wanapitia wanapoingia au kutoka Yerusalema. Uende vilevile kwenye milango yake yote ingine na kutangaza hivi: Musikie neno la Yawe, enyi wafalme wa Yuda, ninyi watu wa Yuda na wakaaji wa Yerusalema ambao wanaopitia kwenye milango hii. Uwaambie kwamba: Yawe anasema hivi: Mufanye angalisho kwa ajili ya maisha yenu. Musibebe muzigo siku ya Sabato, au kuingiza muzigo katika Yerusalema kupitia kwenye milango ya muji. Musibebe muzigo kutoka nyumba zenu siku ya Sabato wala kufanya kazi yoyote. Lakini muihesabu siku ya Sabato kuwa takatifu kama nilivyowaamuru babu zenu. Ingawa hivyo babu zenu hawakunisikiliza wala kunitegea sikio, lakini walifanya vichwa vyao kuwa vigumu, wakakataa kusikia na kufuata maagizo yangu. Lakini ninyi munisikilize mimi. Muache kuingiza muzigo wowote kupitia kwenye milango ya muji huu siku ya Sabato, muihesabu kuwa takatifu na kutofanya kazi. Halafu, wafalme na wana wao watakaotawala nyuma juu ya kiti cha kifalme cha Daudi, wanaopanda juu ya farasi na magari yenye kukokotwa pamoja na watu wa Yuda na wakaaji wa Yerusalema, wataendelea kuingia ndani ya muji huu wakipitia kwenye milango hii. Nao muji huu utaikaliwa na watu siku zote. Watu watakuja kutoka miji ya Yuda na maeneo ya kandokando ya Yerusalema, kutoka inchi ya kabila la Benjamina, kutoka Shefela, kutoka inchi ya milima na kutoka Negebu, wakileta sadaka za kuteketezwa kwa moto na sadaka zingine za kawaida, sadaka ya mavuno na ya ubani wenye harufu nzuri pamoja na matoleo ya shukrani. Hivyo vyote watavileta katika nyumba ya Yawe. Lakini musiponisikiliza na mukiacha kuihesabu siku ya Sabato kama siku takatifu, musipoacha kubeba mizigo na kuingia nayo kupitia milango ya Yerusalema siku ya Sabato, basi nitawakisha moto katika milango yake, nao utateketeza nyumba zote nzuri za Yerusalema, wala hautazimika. –Ni ujumbe wa Yawe. Yawe akanitolea ujumbe, akisema: Yeremia, simama uende kwa nyumba ya mufinyanzi, na huko nitakuambia maneno yangu. Basi, nikatelemuka mpaka kwenye nyumba ya mufinyanzi, nikamukuta mufinyanzi akifanya kazi yake kwenye gurudumu la kufinyangia udongo. Na wakati chombo alichokitengeneza kilipoharibika katika mikono yake, yeye alifinyanga upya chombo kingine kwa kadiri ilivyomupendeza. Kisha neno la Yawe lilinifikia kusema hivi: Enyi Waisraeli! Mimi siwezi kuwafanya ninyi kama mufinyanzi huyu anavyofanya? –Ni ujumbe wa Yawe.– Mujue kwamba kama vile udongo unavyokuwa katika mikono ya mufinyanzi, ndivyo ninyi munavyokuwa katika mikono yangu. Wakati wowote ninaweza kukusudia juu ya taifa au ufalme kwamba nitaliongoa, kulipindua na kuliangamiza. Lakini taifa hilo likigeuka na kuacha uovu wake, basi, mimi nitaacha kulitendea mambo yale niliyokusudia. Vilevile inaweza kunifikia kukusudia wakati wowote juu ya taifa au ufalme fulani kwamba nitalijenga na kulistawisha. Lakini taifa hilo likifanya uovu mbele yangu na kukataa kunitii, basi, mimi nitaacha kulitendea mema hayo niliyokusudia. Basi Sasa, uende kuwaambia watu wa Yuda na wakaaji wa Yerusalema kwamba: Yawe anasema hivi: Mimi nimekwisha kukamata mipango juu yenu, na nimekusudia kuleta hasara juu yenu. Basi kila mumoja arudi kutoka katika njia mbaya, abadilishe mwenendo wake na matendo yake. Lakini wao watasema: Hiyo ni bure tu! Tutafuata mipango yetu wenyewe na kila mumoja wetu atatenda kufuatana na ugumu wa moyo wake mwovu. Basi, Yawe anasema hivi: Muulize habari kwa mataifa yote: Nani amekwisha kusikia jambo kama hili? Kitendo Waisraeli walichokifanya ni cha kuchukiza sana. Teluji ya Lebanoni inatoweka kwenye mawe ya milima ile? Maji ya milima inayoshuka toka kule yanakauka? Lakini watu wangu wamenisahau mimi, wanaifukizia miungu ya uongo ubani. Wamejikwaa katika njia zao, wameacha barabara zao za zamani. Wameifanya inchi yao kuwa kitisho, kuwa kitu cha kuzomewa siku zote. Kila mutu anayepita huko anashangaa na kutikisa kichwa chake. Nitawasambaza mbele ya waadui zao, kama upepo mukali toka mashariki. Nitawageuzia mugongo pahali pa kuwaelekezea uso siku hiyo watakapopatwa na hasara yao. Kisha, watu wakasema: Tuende tufanye shauri baya juu ya Yeremia, maana hatukosi makuhani wa kutufundisha. Vilevile hatukosi watu wenye hekima wa kutushauria na manabii wa kututangazia ujumbe wa Mungu! Mukuje tumushitaki kufuatana na maneno yake mwenyewe, wala tusiyatilie maana mambo yote anayosema. Basi, mimi nikaomba nikisema: Unitegee sikio ee Yawe, usikilize ombi langu. Mutu analipwa mabaya kwa mema? Lakini, wamenichimbia shimo. Kumbuka jinsi nilivyosimama mbele yako, nikasema mema kwa ajili yao, kusudi niepushe hasira yako mbali nao. Kwa hiyo uwaache watoto wao wakufe kwa njaa, uwaache wakufe kwa vita. Wake zao wakuwe tasa na wajane. Waume zao wakufe kwa magonjwa makali na vijana wao wachinjwe kwa upanga katika vita. Kilio kisikilike katika nyumba zao, utakapowaletea kundi la wanyanganyi kwa rafla. Maana wamechimba shimo waninase; wameitegea miguu yangu mitego. Lakini wewe, ee Yawe, unajua mashauri yao ya kuniua. Usiwasamehe uovu wao, wala kufuta zambi zao. Waanguke chini mbele yako; uwapige wakati wa hasira yako. Yawe akaniambia hivi: Kwenda kununua mutungi kwa mufinyanzi. Kisha, uwatwae wakubwa wamoja wa watu na makuhani waongozi wamoja. Halafu uende pamoja nao katika bonde la Mwana wa Hinomu, kwa kupitia mulango unaoitwa mulango wa Vigae. Ukifika huko, utangaze maneno ninayokuambia. Utasema hivi: Musikilize neno la Yawe, enyi wafalme wa Yuda nanyi wakaaji wa Yerusalema. Yawe wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi: Kweli ninaleta hasara kwenye nafasi hii, hata kila mumoja atakayesikia habari ile, atastajabu. Kwa maana watu wameniacha mimi na kuchafua nafasi hii kwa kufukizia miungu mingine ubani; miungu ambayo wao wenyewe, babu zao wala wafalme wa Yuda hawaijui. Zaidi ya ile wamejaza pahali hapa damu ya watu wasiokuwa na kosa, wanamujengea mungu Bali mazabahu, kwa kusudi la kuwachoma wana wao kama sadaka ya kuteketezwa kwa moto kwa ajili ya mungu yule. Mimi sikuwaamuru hata kidogo kufanya vile, wala halikunifikia katika roho. Kwa hiyo, siku zinakuja ambazo nafasi hii haitaitwa tena Tofeti, wala bonde la Mwana wa Hinomu, lakini itaitwa bonde la Mauaji. –Ni ujumbe wa Yawe. Vilevile kwa nafasi hii nitaivuruga mipango ya watu wa Yuda na ya watu wa Yerusalema. Nitawatoa washindwe na kuuawa kwa panga na waadui zao, wale wanaovizia maisha yao. Nazo maiti zao nitaziacha kuwa chakula cha ndege na nyama wa pori. Nitaufanya muji huu kuwa pahali pa kushangaza; nitaufanya kuwa kitu cha kuzomewa. Kila mutu anayepita karibu nao atashangaa na kuuzomea kwa sababu ya hasara zote zitakazowapata. Waadui wao wanavizia maisha yao watauzunguka muji ule kwa vita. Wataleta taabu na masumbuko hata watu watakula wenzao. Nitawafanya wakule miili ya wana na wabinti zao. Kisha wewe utavunja ule mutungi mbele ya watu wale watakaoenda pamoja nawe, na kuwaambia kwamba: Yawe wa majeshi, anasema hivi: Nitavunjavunja watu hawa na muji huu sawa vile mutu anavyovunja chombo cha mufinyanzi, hata kisiweze kutengenezwa tena. Watu watazikwa Tofeti, kwa sababu hapatakuwa pahali pengine pa kuzikia. Vile ndivyo nitakavyotendea nafasi hii na wakaaji wake. –Ni ujumbe wa Yawe.– Nitaufanya muji huu kama Tofeti. Nyumba za Yerusalema na nyumba za wafalme wa Yuda, ndizo nyumba zote ambazo juu ya paa zao watu walifukiza ubani kwa kutambikia makundi ya nyota, na kuitolea miungu mingine sadaka za divai, zote zitageuzwa kuwa chafu kama Tofeti. Nyuma ya mambo haya, Yeremia aliondoka Tofeti, pahali ambapo Yawe alipomutuma aende kutoa unabii, akaenda kusimama katika kiwanja cha nyumba ya Yawe, akawatangazia watu wote maneno haya: Yawe wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi: Mimi nitaleta juu ya muji huu na juu ya vijiji vyote vinavyokuwa kandokando yake hasara zote nilizotangaza juu yake, kwa sababu wakaaji wake ni wenye mioyo migumu, nao wamekataa kusikia maneno yangu. Kuhani Pashuri mwana wa Imeri, ambaye alikuwa musimamizi mukubwa wa nyumba ya Yawe, alimusikia Yeremia akitangaza unabii huo. Basi, Pashuri akamupiga nabii Yeremia na kumutia katika minyororo iliyokuwa upande wa mulango wa juu wa kuingilia katika nyumba ya Yawe, ulioitwa mulango wa Benjamina. Kesho yake asubui, Pashuri akamufungua Yeremia toka minyororo ile. Yeremia akamwambia hivi: Yawe hakuiti tena jina lako “Pashuri”, lakini “Kitisho Kila Pahali”. Maana, Yawe anasema hivi: Nitakufanya ukuwe kitisho kwako wewe mwenyewe na kwa warafiki zako wote. Wao watauawa katika vita kwa upanga wa waadui zao, wewe ukiwa ukiangalia. Nitawatoa watu wote wa Yuda katika mikono ya mufalme wa Babeli, naye atawapeleka kuwa watumwa mpaka Babeli na kuwaua kwa upanga. Zaidi ya hiyo, utajiri wote wa muji, mapato yake yote, vitu vyake vyote vya bei kali pamoja na akiba zote za wafalme wa Yuda, nitavitoa katika mikono ya waadui, ambao watavinyanganya na kuvipeleka Babeli. Na kwa upande wako, wewe Pashuri, pamoja na watu wote wanaokaa ndani ya nyumba yako, mutapelekwa katika utumwa. Hakika mutakwenda Babeli na huko ndiko utakapokufia na kuzikwa, pamoja na warafiki zako wote uliowatabiria uongo. Ee Yawe, wewe umenidanganya, nami kweli nimedanganyika; wewe una nguvu kuliko mimi, nawe umeshinda. Nimekuwa mutu wa kuchekelewa kila siku, kila mutu ananizarau. Kila mara ninaposema kitu, ninalalamika, ninapandisha sauti kwa kutangaza mateso na uharibifu. Kutangaza neno la Yawe kunaniletea kuzomewa na kuzarauliwa kila siku. Lakini ninaposema “Sitamutaja tena Yawe, wala sitasema tena kwa jina lake”, ndani yangu kunawaka kitu kama moto uliofungiwa ndani ya mifupa yangu. Ninajaribu sana kuuzuia humo, lakini ninashindwa. Ninasikia watu wengi wakinisingizia uongo, nao wananipanga jina la Kitisho Kila Pahali! Wengine wanasema: Tumushitaki, Tumushitaki! Rafiki zangu wapenzi wote wanangojea kwa hamu nianguke! Wanasema: Labda atadanganyika, tupate kumunasa na kumulipiza kisasi. Lakini wewe Yawe uko pamoja nami. Kwangu wewe ni kama shujaa wa kutisha. Kwa hiyo watesaji wangu watajikwaa, nao hawataweza kunishinda. Watafezeheka kabisa, kwa sababu hawatashinda. Haya yao itadumu hata milele, nayo haitasahauliwa. Ee Yawe wa majeshi, wewe unayemupima mutu wa haki, unayechunguza mioyo na akili ya watu, nione kisasi chako juu yao maana ninakutegemea kwa kunitetea. Mumwimbie Yawe, mumusifu Yawe, kwa maana anaokoa maisha ya mukosefu kutoka katika mikono ya watu waovu. Ilaaniwe siku niliyozaliwa! Siku hiyo mama aliponizaa, isitakiwe baraka! Alaaniwe mutu aliyemujaza baba yangu furaha kwa kumupelekea ujumbe kwamba amepata mutoto mwanaume. Mutu huyo akuwe kama miji Yawe aliyoiangusha bila huruma. Mutu huyo asikie kilio asubui, na muchana asikie kelele za vita, kwa sababu hakuniua ndani ya tumbo la mama yangu; mama yangu angekuwa kaburi langu, mimba yake ingekuwa ya siku zote. Kwa nini nilitoka katika tumbo la mama yangu? Nilitoka kusudi nipate taabu na huzuni na kuishi maisha ya haya? Neno hili lilimufikia Yeremia kutoka kwa Yawe, wakati mufalme Zedekia alipowatuma Pashuri mwana wa Malkia, na kuhani Zefania mwana wa Masea kwa kumwambia Yeremia hivi: Tafazali, utuombee kwa Yawe, maana Nebukadneza mufalme wa Babeli anaanza kupigana vita nasi. Labda Yawe atatufanyia mumoja wa miujiza yake na kumurudisha Nebukadneza aache kutushambulia. Yeremia akawajibu wale wajumbe: Muende kumwambia Zedekia kwamba: Yawe, Mungu wa Israeli, anasema hivi: Zedekia, nitakugeuzia wewe mwenyewe silaha unazozitumia kwa kupigana na mufalme wa Babeli na waaskari wake wanaozunguka inje ya kuta za muji wenu. Nitazikusanya silaha zile katikati ya muji huu. Mimi mwenyewe nitapigana nawe kwa mukono wangu wenye nguvu na uwezo, kwa hasira, ukali na kasirani kubwa. Nitawaua wakaaji wa muji huu: wanadamu na nyama vilevile. Watakufa kwa magonjwa makali sana. Kisha, wewe Zedekia, mufalme wa Yuda, pamoja na wakubwa wa serikali yako na watu wa muji huu ambao watakaoponyoka magonjwa hayo makali pamoja na vita na njaa, nitawatoa katika mikono ya Nebukadneza, mufalme wa Babeli na katika mikono ya waadui zenu wanaovizia maisha yao. Nebukadneza atawaua kwa upanga wala hatawahurumia au kuwaachilia au kuwasamehe. –Ni ujumbe wa Yawe. Nawe Yeremia utawaambia watu hawa kwamba: Yawe anasema hivi: Musikilize! Mimi ninaweka mbele yenu njia ya uzima na njia ya kifo. Mutu atakayebaki katika muji huu atauawa kwa vita au kwa njaa au kwa magonjwa makali. Lakini mutu atakayetoka inje ya muji huu na kujitoa kwa Wababeli wanaozunguka ukuta wake, ataishi; kweli ataokoa maisha yake. Nimeamua kuleta hasara juu ya muji huu wala siyo mema. –Ni ujumbe wa Yawe.– Nitautoa katika mikono ya mufalme wa Babeli, naye atauteketeza kwa moto. Utaiambia jamaa ya mufalme wa Yuda hivi: Musikilize neno la Yawe! Enyi jamaa ya Daudi, Yawe anasema hivi: Kila asubui muamue maneno kufuatana na sheria yangu, muwakomboe wote walionyanganywa mali zao toka katika mikono ya watesaji. Kama si vile, hasira yangu itawaka kama moto, wala hakuna atakayeweza kuizimisha, kwa sababu ya matendo yenu maovu. Sasa mimi nitapigana nanyi: ninyi munaoishi katika bonde, munaokaa kwenye mawe katika uwanja, ninyi munaosema: Nani atasubutu kutushambulia? Nani anayeweza kuingia katika makao yetu? Nitawaazibu kadiri ya matendo yenu. Nitawakisha moto katika pori lenu nao utateketeza kila kitu kinachokuwa kando yenu. –Ni ujumbe wa Yawe. Yawe anasema hivi: Kwenda kwa jamaa ya kifalme ya Yuda, na utoe ujumbe huu kule: Wewe mufalme wa Yuda unayetawala kwa kiti cha kifalme cha Daudi pamoja na wakubwa wa serikali yako na watu wako wanaopita katika milango hii, musikilize neno la Yawe. Yawe anasema hivi: Mufuate sheria yangu na kutenda kwa haki. Muokoe kila mutu aliyenyanganywa mali zake toka katika mikono ya mutesaji. Musiwatendee vibaya au kwa ukali wageni, wayatima na wajane, wala musimwange damu ya mutu asiyekuwa na kosa kwa nafasi hii. Kama mukishika neno hili nililowaambia, basi wafalme watakaotawala kwa kiti cha kifalme cha Daudi wataendelea kuingia wakipitia milango ya nyumba hii ya kifalme. Watapita pamoja na wakubwa wa serikali yao na watu wao, wakipanda juu ya farasi na magari yenye kukokotwa na farasi. Lakini kama hamutatii maneno haya, ninaapa kwa nafsi yangu mwenyewe kwamba nafasi hii itakuwa mabomoko. –Ni ujumbe wa Yawe. Yawe anasema hivi juu ya nyumba ya kifalme ya Yuda: Ingawa unaonekana vizuri kama inchi ya Gileadi, kama vichwa vya milima ya Lebanoni, ninaapa kwamba nitakufanya kuwa jangwa, ukuwe muji usiokaliwa na watu. Nitawatayarisha waangamizaji wakufikie, kila mumoja akishika silaha yake. Watazikata nguzo zako nzuri za mierezi, na kuzitumbukiza katika moto. Na watu wengi wa mataifa watapita karibu na muji huu, kila mumoja atamwuliza mwenzake: Kwa nini Yawe ameutendea muji huu mukubwa hivi? Nao watajibiana hivi: Ni kwa sababu wakaaji wake walivunja agano la Yawe, Mungu wao, wakaabudu miungu mingine na kuitumikia. Musimulilie yule aliyekufa, musiomboleze kwa ajili yake. Lakini mumulilie kwa uchungu yule anayekwenda mbali kwa sababu hatarudi tena kuiona inchi yake. Maana, Yawe anasema hivi juu ya Salumu mwana wa Yosia, mufalme wa Yuda aliyetawala kwa pahali pa baba yake Yosia, na ambaye aliondoka pahali hapa: Salumu hatarudi tena pahali hapa, lakini atakufia kulekule alipelekwa katika utumwa. Yeye hataiona tena inchi hii. Ole kwako Yoyakimu, wewe unayejijengea nyumba kwa njia isiyokuwa ya haki, na kuiwekea magorofi kwa njia isiyofuata sheria ya Mungu. Unayewatumikisha watu bure pasipo kuwalipa mishahara yao. Wewe unayesema: Nitajijengea nyumba kubwa, yenye vyumba vikubwa vya magorofi. Kisha unaifanyia madirisha, ukafunika kuta zake kwa mbao za mierezi, na kuipaka rangi nyekundu! Unazani umekuwa mufalme kwa kujenga na mierezi? Baba yako alikula na kunywa, alifuata sheria yangu na kutenda mambo ya haki, na mambo yake yaliendeka vizuri. Aliwapatia haki wamasikini na wakosefu, na mambo yake yaliendeka vizuri. Si hivi ndivyo kunijua mimi? –Ni ujumbe wa Yawe.– Lakini macho yako wewe na moyo wako, vinaelekea tu mapato yasiyokuwa ya haki. Unamwanga damu ya wasiokuwa na kosa, nawe unawatesa watu na kuwatendea kwa ukali. Kwa hiyo, Yawe anasema hivi juu ya Yoyakimu mwana wa Yosia, mufalme wa Yuda: Wakati atakapokufa, hakuna atakayeomboleza juu yake, akisema: Yowe, ndugu yangu! Yowe, dada yangu! Wala hakuna atakayemulilia, akisema: Yowe, bwana wetu! Yowe, muheshimiwa wetu! Yeye atazikwa sawa nyama: atakokotwa na kutupiliwa mbali, inje ya milango ya Yerusalema. Enyi watu wa Yerusalema, mupande kwa milima ya Lebanoni mupige kelele, munyanyue sauti zenu huko kwenye uwanja wa Basani; mulalamike kutoka milima ya Abarimu, maana wapenzi wenu wote wameangamizwa. Yawe aliongea nanyi mulipokuwa katika ustawi, lakini ninyi mukasema: Hatutasikiliza. Hii ndiyo tabia yenu tangu utoto wenu, hamujatii sauti ya Yawe. Waongozi wenu watapeperushwa na upepo, wapenzi wenu watapelekwa katika uhamisho. Halafu mutapata haya na kufazaika, kwa sababu ya uovu wenu wote. Enyi wakaaji wote wa Lebanoni, ninyi munaokaa salama kati ya miti ya mierezi, mutaugua sana wakati mutakaposhikwa na uchungu unaokuwa kama wa mwanamuke anayezaa! Yawe anasema hivi: Kama vile ninavyoishi, hata kama wewe Konia mwana wa Yoyakimu, mufalme wa Yuda, ungekuwa wa lazima kwangu kama vile pete yangu ya muhuri ninayovaa kwa mukono wangu wa kuume, ningekuvua. Nitakutoa katika mikono ya wale wanaovizia maisha yako, ndiyo mikono ya wale unaowaogopa, hata katika mikono ya Nabukadneza, mufalme wa Babeli na watu wake. Nitakupeleka mbali katika inchi ya kigeni, wewe pamoja na mama yako muzazi. Mutakuwa watumwa katika inchi hiyo ambamo ninyi wote wawili hamukuzaliwa, nanyi mutakufia kulekule. Mutatamani kwa hamu kubwa kurudi katika inchi hii, lakini hamutarudi. Mbona huyu mutu Konia, amekuwa kama chungu kilichovunjika, ambacho kinazarauliwa na kutupwa inje? Kwa nini yeye na watoto wake wamefukuzwa, wametupwa katika inchi wasiyoijua? Ee inchi, ee inchi, ee inchi! Sikia neno la Yawe! Yawe anasema hivi: Muandike mutu huyu kwamba hana watoto, ni mutu ambaye hatafanikiwa katika maisha yake. Maana hakuna hata mumoja wa wazao wake atakayekiikalia kiti cha kifalme cha Daudi na kutawala tena katika Yuda. Ole kwa wachungaji wanaowaangamiza na kusambaza kundi langu la kondoo! –Ni ujumbe wa Yawe. Yawe, Mungu wa Israeli, anasema hivi juu ya wachungaji wanaowachunga watu wangu: Ninyi munasambaza kondoo wangu na kuwafukuza, wala hamukuwatunza. Basi, nami vilevile nitawaazibu kwa ajili ya matendo yenu maovu. –Ni ujumbe wa Yawe.– Kisha, nitawakusanya kondoo wangu waliobaki kutoka inchi zote nilipowafukuza, na kuwarudisha katika malisho yao. Nao watazaa na kuongezeka. Nitawapa wachungaji watakaowatunza vema, nao hawatakuwa na woga tena wala kufazaika, na hakuna hata mumoja wao atakayepotea. –Ni ujumbe wa Yawe. Siku zinakuja ambapo nitaotesha kichipukizi cha haki toka kizazi cha Daudi. Huyo atatawala kama mufalme, atatenda kwa hekima naye ataimarisha sheria yangu na haki katika inchi. Katika siku za utawala wake, inchi ya Yuda itaokolewa na inchi ya Israeli itakuwa katika usalama. Naye ataitwa kwa jina la Yawe Ni Haki Yetu. Kwa hiyo, siku zinakuja siku ambapo watu hawataapa tena, wakisema: Kama vile Yawe anavyoishi, yule aliyewaondoa watu wa Israeli kutoka katika inchi ya Misri. Lakini wataapa wakisema: Kama vile Yawe anavyoishi, yule aliyewaondoa na kuwaongoza Waisraeli kutoka inchi ya kaskazini na kutoka inchi zote ambapo alipowafukuza. Na halafu wataishi katika inchi yao wenyewe. –Ni ujumbe wa Yawe. Ujumbe juu ya manabii wasiofaa. Nimevunjika moyo, mifupa yangu yote inatetemeka; nimekuwa kama mulevi, kama mutu anayetabanika na pombe, kwa sababu ya Yawe na maneno yake matakatifu. Maana, inchi imejaa wazinzi. Kwa sababu ya laana, inchi inaomboleza, na mashamba ya kulishia nyama yamekauka. Mienendo ya watu ni miovu, wanapoteza nguvu kwa ajili ya mambo yasiokuwa ya haki. Manabii na makuhani, wote hawamwogopi Mungu, uovu wao nimeuona hata ndani ya nyumba yangu. –Ni ujumbe wa Yawe. Kwa hiyo njia zao zitakuwa zenye utelezi na giza, watajigonga na kuanguka; maana, nitaleta hasara juu yao mwaka wa kuwaazibu utakapotimia. –Ni ujumbe wa Yawe. Kati ya manabii wa Samaria, nimeona jambo la kuchukiza sana: nao walitabiri kwa jina la mungu Bali na kupotosha watu wangu Waisraeli. Lakini kati ya manabii wa Yerusalema, nimeona mambo ya kutisha zaidi: wao wanafanya uzinzi na kusema uongo; wanawaunga mukono wanaotenda maovu hata kusikuwe mutu anayeachana na uovu. Kwangu wote wamekuwa kama watu wa Sodoma; wakaaji wake wamekuwa kama watu wa Gomora. Kwa hiyo, Yawe wa majeshi anasema hivi juu ya manabii wa Yerusalema: Nitawakulisha uchungu, na kuwapa maji yenye sumu wakunywe. Maana kutoka kwa manabii wa Yerusalema kutomwogopa Mungu kumeenea kila pahali katika inchi. Yawe wa majeshi anasema hivi: Musisikilize maneno manabii wanaowatabiria; wanawapa matumaini ya uongo. Yale wanayowaambia ni maono ya mioyo yao wenyewe. Hayakutoka katika kinywa cha Yawe. Wanawaambia hivi wale wanaozarau neno langu mimi Yawe: Mambo yenu yataendelea vizuri. Na wanamwambia hivi kila mutu anayefuata ugumu wa moyo wake na mawazo yake: Hakuna hasara yoyote itakayokupata! Lakini ni nani kati ya manabii hao aliyehuzuria katika baraza la Yawe, hata akasikia na kuelewa neno lake? Au ni nani aliyejali neno lake, hata akalielewa? Angalia, zoruba kali kutoka kwa Yawe; kasirani yake imeamuka, upepo mukali utapiga kichwa cha mwovu. Hasira ya Yawe haitatulia, mpaka atakapotimiza na kukamilisha mapenzi ya moyo wake. Kutakuja siku ambapo mutaelewa vema mambo hayo. Yawe anaendelea kusema: Mimi sikuwatuma hao manabii, lakini wao walikwenda mbio; sikuwaambia kitu chochote, lakini wao walitabiri! Kama wangalihuzuria katika baraza langu, wangalitangazia watu wangu maneno yangu, wangaliwageuza kutoka katika njia zao mbaya, na kutoka katika matendo yao maovu. Mimi ni Mungu wa karibu, wala si Mungu wa mbali. –Ni ujumbe wa Yawe.– Mutu anaweza kujificha pahali pa siri hata nisiweze kumwona? –Ni ujumbe wa Yawe!– Hamujui kwamba niko kila pahali, katika mbingu na katika dunia? –Ni ujumbe wa Yawe!– Mimi nimeyasikia maneno waliyosema hao manabii wanaotabiri uongo kwa jina langu, wakisema: Nimeota ndoto, nimeota ndoto! Itakuwa hivyo mpaka wakati gani? Hao manabii wataendelea mpaka wakati gani kupotoka moyo, kutabiri uongo na udanganyifu wao wanaojitungia wenyewe? Kwa ndoto hizo zao wanafikiri kwamba watawashawishi watu wangu wanisahau mimi kama vile babu zao walivyonisahau, na kumufuata mungu Bali! Nabii aliyeota ndoto, atangaze ndoto yake, lakini yule aliyefunuliwa ujumbe wangu autangaze kwa uaminifu. Kuna ulinganifu gani kati ya maganda na ngano? –Ni ujumbe wa Yawe.– Neno langu ni kama moto. –Ni ujumbe wa Yawe!– Neno langu ni kama nyundo inayovunja mawe vipandevipande. Kwa hiyo, mimi nitawashambulia manabii. –Ni ujumbe wa Yawe!– Wanadanganyana kwamba nimetoa ujumbe kwao. Kweli mimi nitawashambulia manabii. –Ni ujumbe wa Yawe! Wanajitungia maneno yao wenyewe na kusema “Ni ujumbe wa Yawe”. Vilevile mimi Yawe ninasema kwamba nitawashambulia manabii wanaotabiri ndoto zao za uongo kwa watu wangu, na kuwapotosha kwa uongo wao na upuuzi wao. Mimi sikuwatuma wala kuwaamuru waende, kwa hiyo hawatawafalia watu hao kitu. –Ni ujumbe wa Yawe! Yawe akaniambia: Mutu yeyote, akuwe nabii au kuhani akikuuliza “Uko wapi muzigo Yawe anaotubebesha?”, wewe utawaambia: Ninyi ndio muzigo kwa Yawe, naye atawatupa mbali. –Ni ujumbe wa Yawe!– Tena nabii au kuhani, au mutu yeyote atakayesema: “Muzigo wa Yawe”, nitamwazibu pamoja na jamaa yake yote. Kitu munachopaswa kuulizana ninyi kwa ninyi ni hiki: “Yawe amejibu nini?” au, “Yawe amesema nini?” Lakini jambo la “Muzigo wa Yawe”, musilitaje tena. Neno mwanadamu analosema litakuwa muzigo kwake mwenyewe, kwa maana munageuza maneno yangu mimi Mungu Mwenye Uzima, Yawe wa majeshi, Mungu wenu. Basi mukiuliza neno kwa nabii, museme hivi: Yawe amekujibu nini? au, Yawe amesema nini? Lakini wao wakivunja amri yangu na kuendelea kusema Muzigo wa Yawe, wakati ambapo mimi niliwakataza wasiseme vile. Basi, uwaambie mimi nitawanyanyua na kuwatupilia mbali, wao wenyewe pamoja na muji niliowapa wao na babu zao. Nitawafanya wafezeheke hata milele na kupata haya ya kudumu ambayo haitasahaulika. Ilikuwa nyuma ya Nebukadneza mufalme wa Babeli kuwahamisha Yekonia mufalme wa Yuda mwana wa Yoyakimu, pamoja na wakubwa wa inchi ya Yuda na wafundi bora na wafuaji wa vyuma kutoka Yerusalema na kuwapeleka Babeli. Yawe akanionyesha vikapu viwili vya matunda ya tini vimewekwa mbele ya hekalu la Yawe. Ndani ya kikapu cha kwanza kulikuwa tini nzuri sana, kama vile tini za mavuno ya kwanzakwanza. Lakini ndani ya kikapu cha pili kulikuwa tini mbaya sana, mbaya hata hazifai kukuliwa. Basi, Yawe akaniuliza: Yeremia! Unaona nini? Mimi nikamujibu: Ninaona tini. Zile nzuri ni nzuri sana, na zile mbaya ni mbaya sana hata hazifai kukuliwa. Halafu neno la Yawe lilinifikia kusema hivi: Yawe, Mungu wa Israeli, anasema hivi: Kama tini hizi zinavyokuwa nzuri, ndivyo nitakavyowaona kuwa wema watu wa Yuda ambao niliowaondoa toka nafasi hii na kuwapeleka katika uhamisho katika inchi ya Wababeli. Nitawalinda siku zote na kuwarudisha katika inchi hii. Nitawajenga, wala sitawabomoa; nitawapanda, wala sitawaongoa. Nitawapa moyo wa kujua kwamba mimi ndimi Yawe. Watakuwa watu wangu, nami nitakuwa Mungu wao; maana watanirudilia kwa moyo wao wote. Yawe anasema hivi: Na kama vile wanavyozitendea zile tini mbaya, tini zinazokuwa mbaya hata hazifai kukuliwa, ndivyo nitakavyowatendea mufalme Zedekia wa Yuda, wakubwa wa serikali yake pamoja na watu wengine wote wa Yerusalema waliobaki katika inchi hii, na vilevile wale ambao walihamia katika inchi ya Misri. Nitawafanya kuwa kitu cha kuchukiza mbele ya falme zote za dunia. Watakuwa kitu cha zihaka, kitu cha kuzomewa, kuchekelewa na kulaaniwa kila fasi nitakapowasambaza. Na zaidi ya ile nitawaletea vita, njaa na magonjwa makali mpaka waangamizwe kabisa kutoka katika inchi niliyowapa wao na babu zao. Katika mwaka wa ine wa utawala wa mufalme Yoyakimu mwana wa Yosia, juu ya inchi ya Yuda, Yawe alimupa Yeremia ujumbe juu ya watu wa Yuda. Mwaka huo ulikuwa wa kwanza wa utawala wa Nebukadneza mufalme wa Babeli. Yeremia akawaambia ujumbe huo watu wote wa Yuda na wakaaji wa Yerusalema, akisema: Kwa muda wa miaka makumi mbili na tatu sasa, ni kusema tangu mwaka wa kumi na tatu wa utawala wa mufalme Yosia, mufalme wa Yuda, mwana wa Amoni, mpaka hivi leo, nimekuwa nikipata neno la Mungu na kulitoa kwenu kila wakati, lakini ninyi hamukusikiliza. Hamukutaka kusikiliza wala kutega sikio, ingawa Yawe aliwaletea watumishi wake manabii kila wakati. Wao waliwaambia hivi: Kila mumoja wenu aachane na mwenendo wake mwovu na matendo yake mabaya, kusudi mupate kuishi katika inchi ambayo Yawe amewapa ninyi na babu zenu tangu zamani kuwa urizi wenu milele. Musifuate miungu mingine wala kuitumikia na kumukasirikisha kwa kuabudu sanamu, nami sitawatendea ubaya wowote. Lakini mulikataa kunisikiliza. Na kisha, mulinikasirikisha na sanamu mulizojitengenezea wenyewe, na kwa hiyo mukajiletea hasara ninyi wenyewe. –Ni ujumbe wa Yawe. Kwa hiyo Yawe wa majeshi anasema hivi: Kwa sababu hamukuyatii maneno yangu, basi, nitayaita makabila yote ya kaskazini pamoja na mutumishi wangu Nebukadneza, mufalme wa Babeli. –Ni ujumbe wa Yawe.– Nitawaleta waishambulie inchi hii na wakaaji wake pamoja na mataifa yote jirani. Nitawaangamiza kabisa, na kuwafanya kuwa kitu cha kuchukiza, cha kuzomewa na kuzarauliwa milele. Tena, nitakomesha toka kati yao sauti za furaha, sauti za wenye kufanya ndoa, wala sauti za kusaga hazitasikilika, wala mwangaza wa taa hautaonekana. Inchi hii yote itakuwa katika mabomoko matupu na ukiwa, na mataifa jirani yatamutumikia mufalme wa Babeli kwa muda wa miaka makumi saba. Hiyo miaka makumi saba itakapopita, nitamwazibu mufalme wa Babeli pamoja na taifa lake. Nitaiangamiza inchi hiyo ya Wababeli. –Ni ujumbe wa Yawe.– Nitafanya hivyo kwa sababu ya uovu wao na kuifanya inchi ibaki mabomoko hata milele. Nitaleta juu ya inchi hiyo mambo yote niliyosema juu yake na yote yaliyoandikwa katika kitabu hiki ambayo Yeremia alitabiri juu ya mataifa yote. Wababeli nao vilevile watakuwa watumwa wa mataifa mengine na wafalme wengine. Nitawaazibu kwa kadiri ya maovu yao waliyotenda. Yawe, Mungu wa Israeli, akaniambia hivi: Twaa toka katika mukono wangu kikombe hiki cha divai kinachojaa kasirani yangu uyakunyweshe mataifa yote ninayokutuma kwao. Mataifa hayo yatakunywa na yatashikwa na kizunguzungu na kupoteza akili kwa sababu ya mauaji nitakayosababisha kati yao. Basi, nikatwaa kikombe hicho toka mukono wa Yawe, nikayakunywesha mataifa yote ambayo Yawe alinituma kwao. Kwanza nikakunywesha wakaaji wa Yerusalema na miji mingine ya Yuda, wafalme wake na wakubwa wa serikali yake kusudi ikuwe jangwa, ukiwa, kitu cha kuzomewa na cha kulaaniwa, kama inavyokuwa mpaka leo. Halafu nikakunywesha: Mufalme wa Misri, wasimamizi wake na wakubwa wa serikali yake pamoja na watu wake wote; wageni wote walioishi katika inchi ya Misri; wafalme wote wa inchi ya Uzi; wafalme wote wa miji ya Wafilistini, Askeloni, Gaza, Ekuroni na mabaki ya Asidodi; watu wote wa Edomu, Moabu na Amoni; wafalme wote wa Tiro na Sidona; wafalme wa inchi zinazokuwa kandokando ya bahari ya Mediteranea; wakaaji wa Dedani, Tema, Buzi na watu wote wanaonyoa nywele zote za pembenipembeni ya kichwa; wafalme wote wa Arabia; wafalme wote wa makabila yanayokaa katika jangwa; wafalme wote wa Simuri, Elamu na Medi; wafalme wote wa kaskazini, wanaokuwa mbali na karibu, mumoja kisha mwingine. Hivi nikakunywesha falme zote za ulimwengu. Na kwa mwisho naye mufalme wa Babeli akakunywa. Yawe akaniamuru: Utawaambia kwamba: Yawe wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi: Mukunywe, mulewe na kutapika; muanguke wala musisimame tena, kwa sababu ya mauaji nitakayosababisha kati yenu. Kama wakikataa kukipokea kikombe hicho utakachowapatia kwa kunywa, utasema hivi: Yawe wa majeshi anasema hivi: Ni lazima mukunywe! Ikiwa ninaanza kuleta hasara katika muji unaojulikana kwa jina langu, basi ninyi munazani kwamba munaweza kuepuka azabu? Hamutaachwa bila kuazibiwa, maana ninaleta mauaji juu ya wakaaji wote wa dunia. –Ni ujumbe wa Yawe. Basi, wewe Yeremia utatabiri maneno haya yote juu yao, na kusema hivi: Yawe atanguruma kutoka juu, atatoa sauti yake kutoka kwenye makao yake matakatifu; atanguruma kwa nguvu kwa ajili ya watu wake, atapiga kelele kama wenye kukamua zabibu, kwa ajili ya wakaaji wote wa dunia. Vishindo hivyo vitasikilika mpaka mwisho wa dunia, maana Yawe ana mashitaki juu ya mataifa; anawahukumu wanadamu wote, naye atawaua waovu kwa upanga! –Ni ujumbe wa Yawe. Yawe wa majeshi anasema hivi: Hasara italifikia taifa kwa taifa, na zoruba itavuma kutoka miisho ya dunia. Siku hiyo, wale watakaouawa na Yawe watasambaa kutoka upande mumoja wa dunia mpaka upande mwingine. Hakuna atakayeomboleza juu yao, wala maiti zao hazitakusanywa wala kuzikwa; zitabaki sawa mboleo juu ya udongo. Muomboleze, enyi wachungaji; mulie na kugaagaa katika majivu, enyi wakubwa wa kundi. Siku za kuchinjwa kwenu na kusambazwa zinakaribia. Mutauawa kama kondoo dume wanene. Wachungaji hawana makimbilio, wakubwa wa kundi hawataweza kutoroka. Musikilize kilio cha wachungaji na malalamiko ya wakubwa wa kundi! Yawe anayaharibu mashamba yao ya malisho. Mashamba ya malisho yaliyostawi vizuri yameharibiwa, kwa sababu ya hasira kali ya Yawe. Yawe amewaacha watu wake, kama vile simba anavyoacha pango lake; inchi yao imekuwa jangwa tupu, kwa sababu ya vita na hasira kali ya Yawe. Kwa mwanzo wa utawala wa Yoyakimu mwana wa Yosia, juu ya inchi ya Yuda, Yawe alimwambia Yeremia hivi: Yawe anasema hivi: Simama katika kiwanja cha nyumba ya Yawe, uwatangazie watu wa miji yote ya Yuda wanaofika kuabudu katika nyumba ya Mungu, mambo yote niliyokuamuru kuwaambia, bila kuacha hata neno moja. Labda watayasikiliza na kila mumoja wao ataacha njia yake mbaya. Wakifanya hivyo, nitabadilisha nia yangu juu ya hasara niliyokusudia kuleta juu yao kwa sababu ya matendo yao maovu. Utawaambia kwamba: Yawe anasema hivi: Kama hamutanisikiliza na kufuata sheria zangu nilizowawekea, na kuyajali maneno ya watumishi wangu manabii ambao ninawatuma kwenu kila mara, ingawa hamukuwasikiliza, basi, nitaiharibu nyumba hii kama nilivyoharibu ile ya Shilo, na nitaufanya muji huu kuwa mufano kwa mataifa yote ya dunia yatakaoutumia kwa kutoa laana. Makuhani, manabii na watu wote wakamusikia Yeremia akisema maneno haya katika nyumba ya Yawe. Basi Yeremia alipomaliza kutangaza mambo yote ambayo Yawe aliyomwamuru kutangaza kwa watu wote, makuhani, manabii na watu wote walimukamata na kusema: Wewe unapaswa kuuawa! Kwa nini umetabiri kwa jina la Yawe, ukisema kwamba nyumba hii itaharibiwa kama ile ya Shilo na muji huu utakuwa ukiwa, bila wakaaji? Na watu wote wakamuzunguka Yeremia katika nyumba ya Yawe. Basi, wakubwa wa Yuda waliposikia mambo hayo, wakapanda kutoka kwa nyumba ya mufalme, wakaenda kwenye nyumba ya Yawe, wakaikaa kwenye mulango ulioitwa: “Mulango Mupya”. Kisha makuhani na manabii wakawaambia wakubwa na watu wote: Mutu huyu anastahili hukumu ya kifo, kwa maana ametabiri juu ya muji huu, kama vile ninyi wenyewe mulivyosikia kwa masikio yenu. Halafu Yeremia akawaambia wakubwa na watu wote: Yawe alinituma niwatabirie mambo yote muliyosikia nikisema juu ya hekalu hili na muji huu. Sasa basi, mugeuze mienendo yenu na matendo yenu na kutii sauti ya Yawe, Mungu wenu. Mukifanya hivyo, Yawe atabadilisha nia yake na kuacha kuwaletea hasara aliyokusudia kuleta juu yenu. Lakini mimi niko sasa katika mikono yenu. Munitendee kama vile munavyoona vema na haki. Lakini mujue kwa hakika kwamba mukiniua, mutakuwa mumejiletea laana ninyi wenyewe kwa kumwanga damu isiyokuwa na kosa, na kuleta laana juu ya muji huu na wakaaji wake. Maana, ni kweli kwamba Yawe alinituma niwaambie mambo hayo kusudi muyasikie. Basi wakubwa na watu wote wakawaambia makuhani na manabii: Mutu huyu hastahili hukumu ya kifo. Amesema nasi kwa jina la Yawe, Mungu wetu. Basi, wasimamizi wamoja wa inchi wakasimama na kuwaambia watu waliokuwa wamekusanyika: Katika siku Hezekia alipokuwa mufalme wa Yuda, Mika wa Moreseti aliwatangazia watu wote kwamba Yawe wa majeshi alisema hivi: Sayuni utalimiwa kama shamba, Yerusalema utabaki mabomoko, nao mulima wa hekalu utakuwa pori. Hezekia, mufalme wa Yuda, na watu wote wa Yuda hawakumwua Mika. Hezekia alimwogopa Yawe na kuomba rehema kwake. Naye Yawe akabadilisha nia yake ya kuleta hasara aliyokusudia juu yao. Lakini sisi tuko mbio kwa kujiletea hasara wenyewe. Kulikuwa mutu mwingine vilevile aliyetabiri kwa jina la Yawe. Mutu huyu aliitwa Uria mwana wa Semaya, wa muji wa Kiriyati-Yearimu. Yeye alitabiri juu ya muji huu na juu ya inchi hii sawasawa na maneno yale Yeremia aliyotabiri. Naye mufalme Yoyakimu pamoja na waaskari shujaa wake na wakubwa wote wa serikali yake waliposikia mambo yale Uria aliyosema, mufalme alitaka kumwua. Lakini Uria alipopata habari ile, alishikwa na hofu, akatoroka na kwenda Misri. Mufalme Yoyakimu akamutuma Elnatani mwana wa Akibori, pamoja na watu wengine kwenda Misri. Wao wakamurudisha Uria kutoka Misri, wakamupeleka kwa mufalme Yoyakimu. Mufalme akamwua kwa upanga na maiti yake ikatupwa katika kaburi. Lakini Yeremia alikuwa akilindwa na Ahikamu mwana wa Safamu kusudi asitiwe katika mikono ya watu na kuuawa. Katika mwanzo wa utawala wa mufalme Zedekia mwana wa Yosia juu ya inchi ya Yuda, Yawe alimutolea Yeremia ujumbe, akisema: Yawe aliniambia hivi: Yeremia, ujitengenezee kamba na nira na kuvifungia kwenye shingo. Kisha, upeleke ujumbe kwa mufalme wa Edomu, mufalme wa Moabu, mufalme wa Amoni, mufalme wa Tiro na mufalme wa Sidona. Uutume kwa mukono wa wajumbe waliokuja Yerusalema kwa kumwona Zedekia mufalme wa Yuda. Uwaamuru wajumbe hao wawaambie wakubwa wao kwamba: Yawe wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi: Ni mimi niliyeumba dunia, watu na nyama wanaokuwa ndani yake kwa uwezo wangu na kwa nguvu zangu kubwa. Nami ninaitoa kwa yeyote ninayetaka. Sasa nimetoa inchi zote kwa mutumishi wangu Nebukadneza mufalme wa Babeli. Vilevile nimemupa nyama wa pori wamutumikie. Mataifa yote yatamutumikia yeye, pamoja na mwana wake na mujukuu wake mpaka wakati inchi yake itakapoanguka. Kisha mataifa mengi na wafalme wengi wakubwa watamufanya kuwa mutumwa wao. Lakini kama taifa lolote au utawala wowote hautajiweka chini ya mamlaka ya Nebukadneza mufalme wa Babeli, na kukataa kubeba katika shingo yao zile nira atakazowalazimisha kubeba, basi nitaliazibu taifa hilo kwa vita, njaa na magonjwa makali mpaka nitakapoliangamiza kabisa kwa njia yake. –Ni ujumbe wa Yawe.– Basi, ninyi musiwasikilize manabii wenu, wapiga ramuli wenu, wafasiriaji wenu wa ndoto, waaguzi wenu au wachawi wenu, wanaowaambia kwamba musimutii mufalme wa Babeli. Hao wanawatabiria uongo. Jambo hilo litawasababisha ninyi kuhamishwa mbali na inchi yenu. Nitawafukuza mbali, nanyi mutaangamia. Lakini watu wa taifa lolote litakalobeba kwenye shingo nira mufalme wa Babeli atakayolazimisha kubeba na kumutumikia, nitawaacha wakae katika inchi yao, walime udongo na kuishi humo. –Ni ujumbe wa Yawe. Yeremia akamwambia Zedekia mufalme wa Yuda, mambo hayohayo, akisema: Mukubali kubeba nira mufalme wa Babeli atakayowalazimisha kubeba. Mumutumikie yeye na watu wake, kusudi mupate kuishi. Kwa nini wewe na watu wako munataka kufa kwa vita, njaa na magonjwa makali? Maana, hivi ndivyo Yawe alivyosema juu ya yale yatakayolipata taifa lolote litakalokataa kumutumikia mufalme wa Babeli. Usisikilize maneno ya manabii wanaokuambia kwamba hautamutumikia mufalme wa Babeli, kwa sababu wanakutabiria uongo. Mimi sikuwatuma manabii hao. Lakini wanatabiri uongo kwa jina langu. Kwa hiyo nitawafukuza, nanyi mutaangamia, pamoja na hao manabii wanaowatabiria uongo. –Ni ujumbe wa Yawe. Kisha, Yeremia akawaambia makuhani na watu wote: Yawe anasema hivi: Musiwasikilize manabii wenu wanaowatabiria, wakisema: “Vyombo vya nyumba ya Yawe vinakaribia kurudishwa kutoka Babeli,” kwa maana wanawadanganya ninyi. Musiwasikilize. Mumutumikie mufalme wa Babeli, kusudi mupate kuishi. Kwa nini muji huu ufanywe kuwa mabomoko? Ikiwa wao ni manabii, na ikiwa wana ujumbe kutoka kwa Yawe, basi wamusihi Yawe wa majeshi, kusudi vyombo vilivyobaki katika nyumba ya Yawe na katika nyumba ya mufalme wa Yuda, na katika Yerusalema, visitwaliwe na kupelekwa Babeli. Kwa maana Yawe wa majeshi anasema hivi juu ya nguzo, birika la shaba na misingi ya kuliwekea, vinara na vyombo vingine vilivyoachwa katika muji huu, ambavyo Nebukadneza, mufalme wa Babeli, hakuvichukua wakati alipowapeleka Yekonia mwana wa Yoyakimu, mufalme wa Yuda na waheshimiwa wote wa Yuda na Yerusalema kwenda katika uhamisho. Kweli, Yawe wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi juu ya vile vyombo vilivyoachwa katika nyumba ya Yawe, katika nyumba ya mufalme wa Yuda na katika Yerusalema: Vyombo hivyo vitapelekwa Babeli, navyo vitabaki huko mpaka siku nitakapovishugulikia. Hapo ndipo nitakapovirudisha na kuviweka tena pahali hapa. –Ni ujumbe wa Yawe. Katika mwaka uleule, maana yake mwaka wa ine wa utawala wa mufalme Zedekia juu ya Yuda, katika mwezi wa tano, Hanania, mwana wa Azuri, nabii kutoka muji Gibeoni, alisema nami katika nyumba ya Yawe. Alisema nami mbele ya makuhani na watu wote, akiniambia kwamba Yawe wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi: Nimevunja nira mufalme wa Babeli anayowabebesha. Mbele ya miaka miwili nitavirudisha hapa vyombo vyote vya nyumba ya Yawe ambavyo Nebukadneza, mufalme wa Babeli alivikamata na kuvipeleka Babeli. Vilevile nitamurudisha Yekonia mwana wa Yoyakimu mufalme wa Yuda pamoja na watu wote wa Yuda waliohamishiwa Babeli. Hakika nitaivunja nira mufalme wa Babeli anayowabebesha. –Ni ujumbe wa Yawe. Kisha, nabii Yeremia akamwambia nabii Hanania mbele ya makuhani na watu wote waliokuwa wamesimama katika hekalu la Yawe: Ikuwe hivyo! Yawe afanye hivyo. Yawe ayatimize maneno uliyotabiri, avirudishe hapa vyombo vya nyumba ya Yawe kutoka Babeli pamoja na watu wote waliohamishiwa huko. Lakini sikiliza neno hili ninalokuambia wewe na watu wanaokuwa hapa: Manabii waliotangulia mbele yetu, mimi na wewe, zamani za kale walitabiri kwamba vita, njaa na magonjwa makali vitazipata inchi nyingi na tawala kubwa. Lakini nabii anayetabiri maneno ya amani, anaweza kutambulikana kama ni nabii aliyetumwa na Yawe, wakati mambo aliyotabiri yanapotokea. Nabii Hanania akatwaa ile nira toka katika shingo la nabii Yeremia na kuivunja. Naye Hanania akasema hivi mbele ya watu wote: Yawe anasema hivi: Mbele ya miaka miwili, hivi ndivyo nitakavyovunja nira ambayo mufalme Nebukadneza anayoibebesha mataifa yote. Kisha nabii Yeremia akajiendea. Nyuma ya pale nabii Hanania alipovunja nira kutoka katika shingo la nabii Yeremia, neno la Yawe lilimufikia Yeremia kusema hivi: Kwenda umwambie Hanania kwamba: Yawe anasema hivi: Wewe umevunja nira ya muti, lakini mimi nitatengeneza ingine ya chuma. Yawe wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi: Nimeweka nira ya chuma ya utumwa kwenye shingo la mataifa yote ya pande hizi, yakuwe katika utumwa, nayo yatamutumikia Nebukadneza, mufalme wa Babeli. Nimemupa Nebukadneza hata nyama wa pori wamutumikie. Basi, nabii Yeremia akamwambia nabii Hanania: Sikiliza, Hanania. Yawe hakukutuma, nawe unawafanya watu hawa waamini uongo. Kwa hiyo Yawe anasema hivi: Nitakuondoa katika dunia. Mwaka huuhuu utakufa, kwa sababu umewasukuma watu wamwasi Yawe. Mwaka huohuo, katika mwezi wa saba, nabii Hanania akakufa. Hii ni barua ambayo nabii Yeremia aliyotuma kutoka Yerusalema kwa wasimamizi wa watu waliopelekwa katika uhamisho Babeli pamoja na makuhani, manabii, na watu wote wengine ambao Nebukadneza alikuwa amewachukua kutoka Yerusalema na kuwapeleka kule. Wakati huu ulikuwa nyuma ya kuondoka Yerusalema kwa mufalme Yekonia na malkia mama wa mufalme, matowashi wa mufalme, wakubwa wa inchi ya Yuda na wa Yerusalema, wafundi na wafua vyuma. Barua hii ilitumwa kwa mukono wa Elasa mwana wa Safamu, na Gemaria mwana wa Hilkia, ambao Zedekia mufalme wa Yuda, aliowatuma kwa Nebukadneza mufalme wa Babeli. Nayo iliandikwa hivi: Yawe wa majeshi, Mungu wa Israeli anasema hivi juu ya watu wote aliowatoa wapelekwe katika uhamisho kutoka Yerusalema na kwenda Babeli: Mujijengee nyumba za kukaa. Mulime mashamba, mupande mbegu na kula mazao yake. Muoe, mupate watoto. Muwaoee wana wenu na kuowesha wabinti zenu, nao vilevile wapate watoto. Muongezeke kule wala musipunguke. Mushugulike na kuleta ustawi katika muji ule ambamo nimewahamishia. Muuombee muji huo kwa Yawe, maana ukistawi ninyi vilevile mutastawi. Yawe wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi: Musikubali kudanganywa na manabii wenu na waaguzi wanaokuwa katikati yenu, wala musisikilize ndoto wanazoota. Maana wanawatabiria uongo kwa kutumia jina langu. Mimi sikuwatuma. –Ni ujumbe wa Yawe. Yawe anasema hivi: Mutakapopitisha miaka makumi saba huko Babeli, nitawashugulikia na kuitimiza ahadi yangu ya kuwarudisha kwa nafasi hii. Maana, mimi ninajua mupango ninaokuwa nao juu yenu. –Ni ujumbe wa Yawe.– Nayo mipango yangu ni ya kuwatendea mema wala si mabaya, kusudi mupate kuwa na tumaini katika siku zinazokuja. Kwa hiyo mutakapokuja kunililia na kuniomba, nitawasikiliza. Mutanitafuta mimi na kuniona. Mutakaponitafuta kwa moyo wote, mutaniona. Nitatengeneza upya maisha yenu na kuwakusanya kutoka mataifa yote na pahali pote nilipowasambaza. Nitawarudisha pahali nilipowaondoa wakati nilipowapeleka katika uhamisho. –Ni ujumbe wa Yawe. Ninyi munasema: Yawe ametuinulia manabii huko Babeli. Yawe anasema hivi juu ya mufalme anayetawala katika kiti cha kifalme cha Daudi, na juu ya watu wote wanaokaa katika muji huu, ndio wandugu zenu ambao hawakuondoka kwenda pamoja nanyi katika uhamisho: Nitawatumia vita, njaa na magonjwa makali. Nitawafanya kuwa kama matunda mabaya sana ya tini zisizoweza hata kukuliwa. Nitawashambulia kwa vita, njaa na magonjwa makali. Nitawafanya kuwa kitu cha kuchukiza kwa falme zote za dunia; nitawafanya kuwa mufano wa kutumia kwa kutoa laana. Mutakuwa kitu cha kushangaza, cha kuzarauliwa na cha kuzomewa kati ya mataifa yote nitakapowasambaza. Nitafanya hivyo kwa sababu hamukusikiliza maneno yangu niliyowaambia kila mara kwa njia ya watumishi wangu, manabii, nanyi mukakataa kusikiliza. –Ni ujumbe wa Yawe. Enyi wote niliowaondoa kutoka Yerusalema na kuwapeleka katika uhamisho kule Babeli, musikilize neno langu mimi Yawe. Yawe wa majeshi, Mungu wa Israeli anasema hivi juu ya Ahabu, mwana wa Kolaya na juu ya Zedekia mwana wa Masea, ambao wanawatabiria uongo kwa jina lake: Nitawatoa katika mikono ya Nebukadneza, mufalme wa Babeli, naye atawaua waziwazi mbele ya macho yenu. Kwa sababu jambo hilo litakalowapata, watu wote waliohamishiwa Babeli kutoka Yuda, watatumia mufano huu kwa kutoa laana: Yawe akufanye kama Zedekia na Ahabu, ambao mufalme wa Babeli aliwachoma katika moto. Jambo hili litawafikia kwa sababu wametenda katika Israeli mambo yasiyofanyika. Walizini na wake za jirani zao, na kusema maneno ya uongo kwa jina langu, jambo ambalo mimi sikuwaamuru wafanye. Mimi ninajua hayo. Nimeyashuhudia. –Ni ujumbe wa Yawe. Yawe akaniagiza kumwambia Semaya wa Nehelamu hivi: Yawe wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi: Umejiruhusu kutuma barua kwa wakaaji wote wa Yerusalema na kwa kuhani Zefania, mwana wa Masea na kwa makuhani wengine wote. Katika barua hiyo, ulimwambia Zefania hivi: Yawe amekufanya wewe Zefania kuwa kuhani kwa pahali pa kuhani Yehoyada, kusudi ukuwe mukubwa wa nyumba ya Yawe. Wewe utashugulika na kumutia katika kifungo na kumufunga kwa minyororo mwenda-wazimu yeyote anayetabiri. Kwa nini basi, haukukaripia Yeremia wa muji wa Anatoti ambaye anakutabiria? Maana yeye alituma habari huko Babeli, akisema: Mutabaki katika uhamisho kwa muda murefu, mujenge nyumba za kukalia, mulime mashamba, mupande mbegu na kula mazao yake! Kuhani Zefania akamusomea nabii Yeremia barua hiyo. Neno la Yawe lilimufikia Yeremia kusema hivi: Utume ujumbe huu kwa watu wote wanaokuwa katika uhamisho: Yawe anasema hivi juu ya Semaya wa Nehelamu: Semaya amewatabiria ninyi ingawa mimi sikumutuma na kuwasukuma musadikie uongo. Kwa hiyo nitamwazibu Semaya wa Nehelamu pamoja na wazao wake. Hakuna hata mumoja wa watu wake atakayebaki muzima na kupata kuona mema nitakayowafanyia watu wangu, kwa sababu amesema maneno ya uasi juu ya Yawe. –Ni ujumbe wa Yawe. Hili ni neno lililomufikia Yeremia kutoka Yawe: Yawe, Mungu wa Israeli, anasema hivi: Andika katika kitabu maneno yote ninayokuambia. Maana, siku zinakuja ambapo nitatengeneza upya maisha ya watu wangu wa Israeli na Yuda. –Ni Yawe anayesema.– Nitawarudisha katika inchi niliyowapa babu zao, nao watairizi. Haya ndiyo mambo aliyosema Yawe juu ya watu wa Israeli na Yuda: Yawe anasema hivi: Kumesikilika kilio cha hofu, kweli ni sauti ya kutisha wala si ya amani. Mujiulize sasa na kufahamu: Mwanaume anaweza kuzaa mutoto? Mbona basi, ninamwona kila mwanaume anajikamata kwenye kiuno kama mwanamuke anayesikia maumivu ya kuzaa na nyuso zimebadilika? Kweli, siku hiyo ni kubwa, hakuna ingine kama hiyo; ni siku ya taabu kwa watu wa Yakobo; hata hivyo, wataokolewa toka humo. Siku hiyo itakapofika, nitaivunja nira inayofungiwa katika shingo lao na kukata minyororo yao. Nao hawatakuwa tena watumwa wa wageni, lakini watanitumikia mimi Yawe, Mungu wao pamoja na mufalme wa ukoo wa Daudi ambaye nitakayewasimikia. Usiogope ee Yakobo, mutumishi wangu, wala usifazaike, ee Israeli. –Ni ujumbe wa Yawe.– Maana nitakuokoa toka huko mbali unapokuwa, nitawaokoa wazao wako kutoka katika uhamisho. Utarudi na kuishi kwa amani, wala hakuna mutu atakayekuogopesha. Maana mimi niko pamoja nawe, nipate kukuokoa. –Ni ujumbe wa Yawe.– Nitayaangamiza kabisa mataifa yote, ambayo niliyokusambaza kati yao; lakini sitakuangamiza wewe kabisa. Nitakuazibu kadiri unavyostahili wala sitakuachilia uende bila kukuazibu. –Ni ujumbe wa Yawe. Yawe anasema hivi: Mapigo yako hayaponi, vidonda vyako haviwezi kutunzwa. Hakuna atakayekushugulikia, kidonda chako hakina dawa, wewe hautapona. Wapenzi wako wote wamekusahau; hawajali kitu chochote juu yako. Nimekupiga sawa vile ungekuwa adui yangu. Umeazibiwa bila huruma, kwa sababu kosa lako ni kubwa, zambi zako ni nyingi sana. Kwa nini unalia kwa ajili ya kidonda chako? Maumivu yako hayawezi kupona. Nimekutendea hayo yote, kwa sababu kosa lako ni kubwa, zambi zako ni nyingi sana. Lakini wote wanaokuangamiza, wataangamizwa vilevile, na waadui zako wote watapelekwa katika uhamisho; nao wanaokukamata mateka watakamatwa mateka, nao wanaokuwinda, nitawawinda. Sasa wanakuita wewe Sayuni: “Aliyetupiliwa”, “Muji usioshugulikiwa na mutu”. Lakini nitakurudishia afya yako, nitaponyesha vidonda vyako. –Ni ujumbe wa Yawe. Yawe anasema hivi: Nitatengeneza upya maisha ya jamaa za wazao wa Yakobo, nitayaonea makao yao huruma; muji wao utajengwa upya kwenye mabomoko yake, nyumba ya kifalme itasimama pahali ilipokuwa mbele. Humo mutasikilika nyimbo za shukrani nayo makelele ya wenye kufanya sherehe. Nitawaongeza wala hawatakuwa wachache; nitawafanya waheshimiwe wala hawatazarauliwa. Watoto wao watakuwa kama walivyokuwa zamani, nayo makundi yatasimama imara mbele yangu, nami nitawaazibu wote wanaowagandamiza. Mwongozi wao atakuwa mumoja wao, mutawala wao atatokea katikati yao. Nitamuruhusu kuwa karibu nami; maana, ni nani anayeweza kusubutu kuhatarisha uzima wake kwa kunikaribia? –Ni ujumbe wa Yawe.– Mutakuwa watu wangu, nami nitakuwa Mungu wenu. Angalia, zoruba kali kutoka kwa Yawe! Kasirani yake imeamuka, upepo mukali utapiga kichwa cha mwovu. Hasira ya Yawe haitatulia, mpaka atakapotimiza na kukamilisha mapenzi ya moyo wake. Kutakuja siku ambazo mutaelewa vema mambo hayo. Kutakuja siku ambazo nitakuwa Mungu wa jamaa zote za Waisraeli, nao watakuwa watu wangu. –Ni ujumbe wa Yawe. Yawe anasema hivi: Watu walioponyoka kuuawa, nilionyesha neema yangu kwao katika jangwa. Wakati Israeli alipotafuta kwenda kupumzika, mimi Yawe nilimutokea kwa mbali. Nami nimekupenda kwa mapendo ya milele, kwa hiyo nimeendelea kuwa mwema kwako. Nitakurudisha katika hali mupya, ewe binti Israeli! Utazitwaa tena ngoma zako, nawe utajitokeza tena kwa kucheza na wenye shangwe. Utapanda tena mizabibu juu ya milima ya Samaria; walimaji watapanda mbegu na kuyafurahia mazao yake! Maana kutakuja siku ambapo walinzi watalalamika hivi katika vilima vya Efuraimu: Musimame, tupande kwenda Sayuni kwa Yawe, Mungu wetu. Maana Yawe anasema hivi: Mushangilie kwa furaha kwa ajili ya Yakobo, mupige vigelegele kwa ajili ya taifa kubwa, mutangaze, musifu na kusema: Yawe ameokoa watu wake, ameleta ukombozi kwa wale waliobaki kati ya Waisraeli! Nitawarudisha kutoka inchi ya kaskazini, nitawakusanya kutoka miisho ya dunia. Wote watakuwa pale; hata vipofu na vilema, wanawake wenye mimba na wanaosikia maumivu ya kuzaa; kundi kubwa sana la watu litarudi hapa. Watarudi wakiwa wanatoa machozi, nami nitawaongoza nikiwafariji; nitawapitisha kando ya vijito vya maji, katika njia iliyonyooka ambamo hawatajikwaa; maana mimi nimekuwa baba wa Israeli, Efuraimu ni muzaliwa wangu wa kwanza. Enyi mataifa, musikilize neno langu mimi Yawe, mulitangaze katika visanga vya mbali, museme hivi: Aliyemusambaza Israeli, atamukusanya, atamutunza kama muchungaji anavyotunza kondoo wake. Maana mimi Yawe nimemukomboa Yakobo, nimemwokoa kutoka kwa wenye nguvu kuliko yeye. Watakuja na kuimba kwa sauti juu ya mulima Sayuni, watapata utukufu juu ya wema wangu mimi Yawe, kwa ajili ya ngano, divai na mafuta ninavyowapa, kwa ajili ya kondoo na ngombe vilevile; maisha yao yatakuwa kama bustani iliyotiliwa maji, wala hawataregea tena. Halafu wabinti zao watafurahi na kucheza, vijana na wazee watashangilia kwa furaha. Nitageuza maombolezo yao kuwa furaha, nitawafariji na kuwapa furaha pahali pa huzuni. Nitawashibisha makuhani kwa nyama wenye kunona, watu wangu watatosheka kwa wema wangu. –Ni ujumbe wa Yawe. Yawe anasema hivi: Sauti imesikilika katika muji wa Rama, maombolezo na kilio cha uchungu. Rakeli anawalilia watoto wake, wala hataki kufarijiwa kwa ajili yao, maana wote hawako tena. Yawe anasema hivi: Acha kulia, panguza machozi yako, maana utapata malipo kwa kazi yako. –Ni ujumbe wa Yawe.– Watoto wenu watarudi kutoka inchi ya waadui zenu. Kuna matumaini kwa siku zenu zinazokuja, maana watoto wenu watarudia katika inchi yao. –Ni ujumbe wa Yawe. Nimesikia Efuraimu akilalamika hivi: Umeniazibu vikali, maana nilikuwa kama mwana-ngombe asiyezoea nira. Unigeuze nami nitakugeukia, maana wewe ndiwe Yawe, Mungu wangu. Maana kisha kukuasi, niligeuka toka zambi zangu, na kisha kufundishwa, nilijilaumu, nikapata haya na kufezeheka, maana nilibeba haya za ujana wangu. Efuraimu ni mwana wangu mupendwa; yeye ni mutoto wangu ninayemupenda sana. Ndiyo maana kila mara ninapomutisha, ninaendelea kumukumbuka. Moyo wangu unamwelekea kwa wema; hakika nitamuhurumia. –Ni ujumbe wa Yawe. Weka kitambulisho katika njia zako, simika nguzo za kukuongoza, ukumbuke vema ile njia kubwa, barabara uliyopita ndani yake ukienda. Ewe Israeli rudi, rudi kwa nyumba katika miji yako. Utasitasita mpaka wakati gani, ewe binti usiyekuwa mwaminifu? Maana, mimi nimefanya kitu kipya katika dunia; mwanamuke anamulinda mwanaume. Yawe wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi: Nitakapowafanikisha tena watu wa Israeli, wao watatangaza tena katika inchi ya Yuda na katika miji yake wakisema: Yawe akubariki, ewe makao ya haki; akubariki, ee mulima mutakatifu! Halafu watu wa Yuda na miji yake yote, walimaji na wachungaji wanaopitapita na makundi yao watakaa huko pamoja. Waliochoka nitawachangamusha, na waregevu nitawapa nguvu. Ndiyo maana mutu ataweza kusema hivi: Niliamuka nikatambua kwamba usingizi wangu ulinifalia sana. Siku zinakuja ambapo nitaijaza inchi ya Israeli na inchi ya Yuda watu na nyama kama vile mulimaji anavyopanda mbegu. Na kadiri nilivyokuwa mwangalifu kuwaongoa, kuwabomoa, kuwaangusha, kuwaharibu na kuwatesa, ndivyo nitakavyokuwa mwangalifu kwa kuwapanda na kuwajenga. –Ni ujumbe wa Yawe. Siku hizo watu hawatasema tena: Wazee walikula matunda mabichi ya mizabibu, na meno ya watoto ndiyo yanaumizwa. Lakini kila mumoja atakufa kwa sababu ya zambi zake mwenyewe; ni yule tu atakayekula matunda mabichi ya mizabibu ndiye meno yake yataumizwa. Siku zinakuja ambapo nitafanya agano jipya na watu wa Israeli na watu wa Yuda. Agano hili halitakuwa kama lile nililofanya na babu zao nilipowatoa kwa mukono wangu kutoka Misri; agano hilo walilivunja, ingawa mimi nilikuwa Bwana wao. Kisha siku hizo, nitafanya agano hili na Waisraeli. Nitaiweka sheria yangu ndani yao, na kuiandika katika mioyo yao. Mimi nitakuwa Mungu wao, nao watakuwa watu wangu. Ni mimi Yawe ninayesema hivyo. Wala hawatafundishana tena kila mutu na jirani yake, na kila mutu na ndugu yake na kusema “Mumujue Yawe”, kwa sababu wote, wadogo kama vile wakubwa, watanijua mimi Mungu. Maana nitawasamehe makosa yao, wala sitazikumbuka tena zambi zao. Yawe, yule aliyepanga jua liangaze muchana, mwezi na nyota viangaze usiku, na anayevumisha mawimbi ndani ya bahari, yule ambaye jina lake ni Yawe wa majeshi, anasema hivi: Ikiwa itanifikia kuvunja mipango ile, halafu nitaweza vilevile kukomesha kizazi cha Waisraeli, wasiitwe tena taifa langu siku zote. –Ni ujumbe wa Yawe. Yawe anasema hivi: Kama mbingu zinaweza kupimwa, na misingi ya dunia kuchunguzwa, basi, nitawatupilia wazao wa Israeli, kwa sababu ya mambo yote waliyotenda. Siku zinakuja ambapo muji huu wa Yerusalema utajengwa upya kwa ajili ya Yawe, kutokea kwenye munara wa Hananeli mpaka kwenye mulango wa Pembe. Nayo kamba ya kupima itanyooshwa moja kwa moja mpaka kwenye mulima Garebu, kisha itazungushwa mpaka Goa. Bonde lote walimozikwa wafu na kutupiwa majivu, mashamba yote, mpaka kijito cha Kidroni, mpaka pembe ya mulango wa Farasi kuelekea upande wa mashariki, litakuwa eneo takatifu kwa Yawe. Hakuna kitakachoharibiwa humo wala kubomolewa tena milele. Yawe akamutolea Yeremia ujumbe katika mwaka wa kumi wa utawala wa Zedekia mufalme wa Yuda, ambao ulikuwa mwaka wa kumi na nane wa utawala wa Nebukadneza. Wakati huo, waaskari wa mufalme wa Babeli walikuwa wakizunguka Yerusalema kwa vita, naye nabii Yeremia alikuwa amefungwa katika baraza la walinzi uliokuwa ndani ya nyumba ya mufalme wa Yuda. Maana Zedekia, mufalme wa Yuda, alikuwa amemufunga Yeremia akisema: Kwa nini unatabiri na kusema: Yawe anasema hivi: Mimi ninautia muji huu katika mikono ya mufalme wa Babeli, naye atauteka. Zedekia, mufalme wa Yuda, hataepuka kutiwa katika mikono ya Wakaldea; hakika atatekwa na mufalme wa Babeli, ataonana naye uso kwa uso na kuongea naye kinywa kwa kinywa. Zedekia atapelekwa mpaka Babeli, naye atakaa huko mpaka nitakapomushugulikia. –Ni ujumbe wa Yawe.– Kama mukipigana na Wakaldea, hamutawashinda. Yeremia akasema: Neno la Yawe lilinifikia kusema hivi: Hanameli mwana wa baba yako mudogo Salumu atakuja kwako na kusema: Nunua shamba langu linalokuwa kule Anatoti, maana wewe ni ndugu yangu kabisa, nawe uko na haki ya kulikomboa. Kisha binamu yangu Hanameli akanifikia katika baraza la walinzi kama alivyonifahamisha Yawe, akaniambia: Nunua shamba langu linalokuwa kule Anatoti katika inchi ya Benjamina maana wewe uko na haki ya kulikomboa. Ulinunue kwa faida yako. Basi nikajua kwamba neno hili ni la Yawe. Nikalinunua shamba hilo linalokuwa kule Anatoti, kutoka kwa binamu yangu Hanameli, nikamulipa bei yake vikoroti kumi na saba vya feza. Nikatia sahihi juu ya barua ya ununuzi, nikaipiga muhuri, nikawaita washuhuda na kuipima ile feza juu ya mizani. Kisha, nikakamata ile barua ya ununuzi niliyoipiga muhuri, ambayo ilikuwa na masharti na kanuni, pamoja na barua ingine iliyokuwa wazi. Nilimupa Baruku mwana wa Neria mujukuu wa Masea ile barua ya ununuzi mbele ya binamu yangu Hanameli na washuhuda waliokuwa wametia sahihi juu ya barua ya ununuzi, na mbele ya Wayuda wote waliokuwa wameikaa katika baraza la walinzi. Mbele ya watu wote hao, nikamupa Baruku maagizo haya: Yawe wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi: Twaa barua hizi zote mbili, barua hii ya ununuzi wa shamba iliyotiwa sahihi, na hii ingine inayokuwa wazi, uziweke katika chungu cha udongo kusudi zipate kulindwa kwa muda murefu. Maana Yawe wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi: Nyumba na mashamba, pamoja na mashamba ya mizabibu katika inchi hii yatanunuliwa tena. Kisha kumupatia Baruku mwana wa Neria barua ya ununuzi wa shamba, nilimwomba Yawe nikisema: Ee Bwana wangu Yawe, ni wewe ambaye kwa nguvu zako nyingi na uwezo wako mukubwa, umeziumba mbingu na dunia. Wewe unaonyesha mema yako kwa maelfu ya watu; lakini unawaazibu vilevile watu kwa sababu ya zambi za babu zao. Wewe ni Mungu Mukubwa, mwenye nguvu, Yawe wa majeshi ndilo jina lako. Wewe unapanga kwa hekima na unafanya maajabu; njia za watu wote ziko wazi mbele yako, unamulipa kila mumoja kadiri ya njia zake na matendo yake. Katika inchi ya Misri ulifanya maajabu, ukatenda miujiza, na unaendelea kufanya hivyo mpaka leo kati ya Waisraeli na katika mataifa mengine vilevile, jambo ambalo limekufanya ujulikane kila nafasi. Kwa maajabu na miujiza uliyowatisha nayo Wamisri, uliwatoa watu wako Misri kwa nguvu zako nyingi na uwezo wako mukubwa. Uliwapa inchi hii ambayo uliahidi kuwapa babu zao, inchi inayotiririka maziwa na asali. Nao walifika, wakaitwaa na kuirizi. Lakini wao hawakukusikiliza, wala hawakufuata sheria zako. Hawakutenda mambo uliyoamuru. Ndiyo maana utawafanya wapatwe na hasara hii. Angalia, Wakaldea wamechimba mifereji kuuzunguka muji; wanauzunguka kusudi wapate kuuteka; wanaushambulia. Vita, njaa na magonjwa vitaufanya muji utekwe na watu hao. Kweli mambo uliyotabiri yametokea. Unaona mwenyewe. Lakini, ee Bwana wangu Yawe, wewe ndiwe uliyeniambia: “Nunua shamba kwa feza na kuweka washuhuda”, ingawa muji wenyewe umetekwa na Wakaldea. Neno la Yawe lilimufikia Yeremia kusema hivi: Mimi ni Yawe, Mungu wa watu wote. Hakuna lolote linaloweza kunishinda. Yawe anasema hivi: Kwa hiyo, ninautoa muji huu kwa Wakaldea na kwa Nebukadneza mufalme wa Babeli, naye atauteka. Wakaldea wanaoushambulia muji huu wataingia na kuuteketeza kwa moto; watauteketeza pamoja na nyumba ambazo juu ya paa zake ubani ulifukiziwa kwa mungu Bali na sadaka za divai zilitolewa kwa miungu mingine, kwa kunichokoza. Maana Waisraeli na watu wa Yuda hawakufanya chochote mbele yangu isipokuwa uovu tangu ujana wao; watu wa Israeli hawakufanya chochote isipokuwa kunikasirikisha kwa matendo yao. –Ni ujumbe wa Yawe.– Muji huu umechochea hasira yangu na kuniuzi tangu siku ulipojengwa mpaka leo hii. Kwa hiyo, nitauondoa kabisa mbele yangu, kwa sababu ya uovu wote watu wa Israeli na Wayuda waliotenda, pamoja na wafalme na wakubwa wao, makuhani na manabii wao, na wakaaji wa Yerusalema. Wao walinigeuzia mugongo pahali pa kunigeuzia nyuso zao; ingawa nimewafundisha tena na tena, wao hawakusikiliza na kuyapokea mafundisho yangu. Waliweka sanamu za miungu yao ya kuchukiza katika nyumba hii inayojulikana kwa jina langu, wakaichafua. Walimujengea mungu Bali mazabahu katika bonde la Mwana wa Hinomu, kusudi wamutolee mungu Moleki wana wao na wabinti zao, ingawa sikuwaamuru wala sikufikiria kwamba wangefanya hivyo. Wakasukuma watu wa Yuda watende zambi. Sasa basi, Yawe, Mungu wa Israeli, anasema hivi: Yeremia, watu hawa wanasema kwamba, kwa vita, njaa na magonjwa, muji huu utatiwa katika mikono ya mufalme wa Babeli. Lakini ninasema: Nitawakusanya watu kutoka inchi zote ambako kwa hasira na kasirani na chuki yangu kubwa, niliwatawanya. Nitawarudisha tena hapa, na kuwafanya wakae salama. Nao watakuwa watu wangu, nami nitakuwa Mungu wao. Nitawapa moyo mumoja na nia moja, wapate kuniheshimu mimi siku zote, kwa faida yao wenyewe na kwa faida ya watoto wao watakaofuata. Nitafanya nao agano la milele, kwamba sitaacha kuwatendea mema hata kidogo; nitaweka ndani ya mioyo yao utii kwa ajili yangu kusudi wasiniache tena. Nitafurahi kuwatendea mema; nitawasimika siku zote katika inchi hii na kuwatendea kwa uaminifu. Yawe anasema hivi: Kama nilivyowaletea hasara watu hawa, ndivyo nitakavyowaletea mema niliyowaahidi. Mashamba yatanunuliwa katika inchi hii ambayo unasema imekuwa ukiwa bila watu wala nyama, na kwamba imetolewa kwa Wakaldea. Watu watanunua mashamba kwa feza, watazitia sahihi barua zake za ununuzi, watazipiga muhuri, na kuweka washuhuda katika inchi ya Benjamina, kandokando ya Yerusalema, katika miji ya Yuda, katika miji ya inchi ya milima, katika miji ya Shefela, na katika miji ya jangwa la Negebu. Maana nitawastawisha tena. –Ni ujumbe wa Yawe. Neno la Yawe lilimufikia Yeremia mara ingine, wakati alipokuwa angali amefungwa katika baraza la walinzi, kusema hivi: Yawe aliyeiumba dunia, Yawe aliyeifanya na kuiimarisha dunia, yule ambaye jina lake ni Yawe, anasema hivi: Uniite, nami nitakujibu na kukuambia mambo makubwa yaliyofichwa ambayo haujapata kuyajua. Maana Yawe, Mungu wa Israeli, anasema hivi juu ya nyumba za Yerusalema na nyumba za wafalme wa Yuda zilizobomolewa kwa sababu ya vita. Watu watajaribu kupigana na Wakaldea lakini hiyo itakuwa bure, maana mifereji itajaa maiti za watu ambao nitawaua kwa hasira na kasirani yangu. Kwa vile wamefanya uovu huo wote, mimi nitauacha muji huu. Hata hivyo, mimi nitauponyesha muji huu na kuwapa watu wake afya; nitawajalia ustawi mwingi na usalama. Nitawastawisha tena Wayuda na watu wa Israeli; nitawaimarisha kama walivyokuwa hapo zamani. Nitatakasa zambi zao zote na kuwasamehe uovu wao na uasi walionitendea. Nao muji huu utakuwa kwangu jina la furaha, sifa na utukufu mbele ya mataifa yote katika dunia ambayo yatasikia juu ya mema yote ninayowafanyia. Mataifa yataogopa na kutetemeka kwa sababu ya mema na amani nitakazouletea muji huu wa Yerusalema. Yawe anasema hivi: Katika muji huu ambao munasema kwamba umekuwa ukiwa bila watu wala nyama, katika miji ya Yuda na katika barabara za Yerusalema ambazo ni tupu, bila watu wala nyama, humo kutasikilika tena sauti za vicheko, sauti za furaha, sauti za arusi na za furaha, sauti za waimbaji wakati wanaleta sadaka za shukrani katika nyumba ya Yawe. Wataimba hivi: Mumushukuru Yawe wa majeshi kwa sababu Yawe ni muzuri, kwa maana wema wake unadumu milele. Nitairudishia inchi hii hali yake ya zamani. –Ni Yawe anayesema. Yawe wa majeshi anasema hivi: Pahali hapa ambapo ni jangwa bila watu wala nyama, na katika miji yake yote, patakuwa shamba ambalo wachungaji watakulisha ndani yake makundi yao ya kondoo. Katika miji ya inchi yenye milima, katika miji ya Shefela na katika miji ya jangwa la Negebu, katika inchi ya Benjamina, kandokando ya Yerusalema na katika miji ya Yuda, watu watahesabu tena kondoo wao. –Ni Yawe anayesema. Siku zinakuja ambapo nitatimiza ahadi yangu niliyofanya na Waisraeli na Wayuda. Katika siku hizo, katika wakati huo, nitaotesha chipukizi wa haki wa uzao wa Daudi. Chipukizi huyo ataimarisha sheria yangu na haki katika inchi. Wakati huo inchi ya Yuda itaokolewa na Yerusalema utakuwa salama. Na muji huo utaitwa “Yawe ni Ukombozi Wetu”. Maana Yawe anasema hivi: Hakutakosekana hata kidogo mutu wa uzao wa Daudi atakayetawala Waisraeli. Vilevile nao makuhani wa ukoo wa Lawi watakuwa pale siku zote kwa kunitumikia wakinitolea sadaka za kuteketezwa na sadaka za unga na kunitolea sadaka milele. Neno la Yawe lilimufikia Yeremia kusema hivi: Yawe anasema hivi: Kama munaweza kuvunja agano langu nililofanya na usiku na muchana kwa jinsi usiku na muchana visikuwe kwa wakati wake, ndivyo itakuwa kwa agano nililofanya na mutumishi wangu Daudi. Nilifanya agano na Daudi kwamba atakuwa na mumoja wa uzao wake wa kutawala pahali pake siku zote; vilevile kutakuwa makuhani wa ukoo wa Lawi watakaonitumikia siku zote. Kama vile nyota katika anga na muchanga katika bahari visivyoweza kuhesabiwa, ndivyo nitakavyoongeza hesabu ya wazao wa mutumishi wangu Daudi na hesabu ya makuhani wa ukoo wa Lawi. Neno la Yawe lilimufikia Yeremia kusema hivi: Haujasikia namna watu hawa wanavyosema, kwamba mimi Yawe nimewatupilia mbali watu wa Israeli na watu wa Yuda, jamaa mbili nilizochagua? Wamewazarau watu wangu, hata kuwaona kwamba wao si taifa. Yawe anasema hivi: Mimi niliweka agano juu ya muchana na usiku na kuweka maagizo ya mbingu na dunia. Basi, ndivyo inavyokuwa vilevile: sitawatupa wazao wa Yakobo na Daudi, mutumishi wangu; nitamuchagua mumoja kati ya wazao wake atawale wazao wa Abrahamu, Isaka na Yakobo. Kwa maana nitawarudishia tena hali yao na kuwahurumia. Yawe akamutolea Yeremia ujumbe huu wakati Nebukadneza, mufalme wa Babeli, pamoja na waaskari wake wote na falme zote za dunia zilizokuwa chini ya utawala wake, vilevile na watu wote walipokuwa wakiushambulia Yerusalema na miji mingine yote ya kandokando yake: Yawe, Mungu wa Israeli, anasema hivi: Kwenda usemezane na Zedekia, mufalme wa Yuda. Umwambie kwamba mimi Yawe ninasema hivi: Nimeutia muji huu katika mikono ya mufalme wa Babeli, naye atauteketeza kwa moto. Nawe hautatoroka toka mikono yake, lakini kwa hakika utatekwa na kupelekwa kwake; utaonana na mufalme wa Babeli macho kwa macho, na kusema naye kinywa kwa kinywa; kisha, utakwenda Babeli. Lakini, ewe Zedekia, mufalme wa Yuda, sikia ujumbe wa Yawe. Yawe anasema hivi juu yako: Wewe hautauawa kwa upanga katika vita. Utakufa kwa amani. Na kama vile watu walivyochoma ubani walipowazika babu zako waliokuwa wafalme, ndivyo watakavyokuchomea ubani na kuomboleza wakisema: Masikini! Mufalme wetu amekufa! –Ni ujumbe wa Yawe. Kisha, nabii Yeremia akamwelezea Zedekia, mufalme wa Yuda, maneno hayo yote huko Yerusalema, wakati waaskari wa mufalme wa Babeli walipokuwa wanaushambulia Yerusalema na vilevile miji ya Lakisi na Azeka, ambayo ilikuwa miji pekee iliyobaki ikizungukwa na kuta. Huu ndio ujumbe uliotolewa kwa Yeremia kutoka kwa Yawe kisha mufalme Zedekia kufanya agano na watu wote wa Yerusalema kuwaachilia huru watumwa na wajakazi wao wa Kiebrania, kusudi mutu yeyote asimufanye Muyuda mwenzake kuwa mutumwa. Wakubwa wote na watu wote waliofanya agano hilo walikubaliana wote wawaachilie huru watumwa wao na wajakazi, na mutu yeyote asiwafanye tena kuwa watumwa. Walikubaliana, wakawaacha huru. Lakini kisha walibadilisha nia zao, wakawashika tena watumwa na wajakazi hao ambao walikuwa wamewaacha huru, wakawafanya watumwa. Halafu neno la Yawe lilimufikia Yeremia kusema hivi: Yawe, Mungu wa Israeli, anasema hivi: Nilifanya agano na babu zenu nilipowatoa toka inchi ya Misri ambako walikuwa watumwa, nikawaambia: Kila mwaka wa saba, kila mumoja wenu atamwachilia huru ndugu yake Muyuda aliyeuzishwa kuwa mutumwa kwa muda wa miaka sita. Munapaswa kuwaachilia huru, wasiwatumikie tena. Lakini babu zenu hawakunisikiliza wala kunitegea sikio. Hivi karibu siku hizi ninyi mulibadilika, mukafanya mambo yanayokuwa sawa mbele yangu, mukawaachilia huru Waisraeli wenzenu na kufanya agano mbele yangu katika nyumba yangu. Lakini muligeuka, mukachafua jina langu, wakati mulipowakamata tena watumwa na wajakazi walewale ambao mulikuwa mumewaachilia kama walivyotaka, mukawalazimisha kuwa watumwa tena. Kwa hiyo, Yawe anasema hivi: Ninyi hamukunitii juu ya kuwapatia wandugu zenu Waisraeli uhuru. Basi, nami vilevile nitawapatia ninyi uhuru: uhuru wa kuuawa kwa upanga katika vita, kuuawa kwa ugonjwa mukali na kwa njaa. Nitawafanya ninyi kuwa kitambulisho cha kuogopesha kwa falme zote katika dunia. Watu waliovunja agano langu na kukataa kufuata masharti ya agano walilofanya mbele yangu, nitawafanya kama yule mwana-ngombe waliyemukata sehemu mbili na kupita katikati ya vipande vile. Watu hao ndio hao wakubwa wa inchi ya Yuda, wakubwa wa muji Yerusalema, matowashi wa mufalme, makuhani, pamoja na wanainchi wote waliopita katikati ya sehemu mbili za yule mwana-ngombe. Watatiwa katika mikono ya waadui zao, na katika mikono ya watu wanaotaka kuwaua. Maiti zao zitakuliwa na ndege na nyama wa pori. Naye Zedekia, mufalme wa Yuda, pamoja na wakubwa wake, nitawatia katika mikono ya waadui zao, na katika mikono ya watu wanaotaka kuwaua; ni kusema katika mikono ya waaskari wa mufalme wa Babeli ambao wameondoka na kuacha kuwashambulia. Nitawaamuru nao wataurudia katika muji huu. Wataushambulia, watauteka na kuuteketeza kwa moto. Nitaifanya miji ya inchi ya Yuda kuwa ukiwa bila wakaaji. –Ni ujumbe wa Yawe. Yawe akamutolea Yeremia ujumbe huu wakati wa utawala wa Yoyakimu mwana wa Yosia, mufalme wa Yuda: Kwenda kwa wazao wa Rekabu, useme nao. Kisha, uwalete katika chumba kimoja ndani ya nyumba yangu mimi Yawe, uwape divai wakunywe. Basi, nikamutwaa Yazania mwana wa Yeremia mujukuu wa Habazinia na wandugu zake pamoja na wanawake wote na ukoo wote wa Warekabu, nikawaleta kwenye nyumba ya Yawe, katika chumba cha wana wa mutu wa Mungu Hanani mwana wa Igidalia. Chumba hicho kilikuwa karibu na chumba cha wakubwa juu ya chumba cha mulinzi wa mulango Maseya mwana wa Salumu. Kisha nikaleta vikombe na mabakuli yaliyojaa divai mbele ya hao Warekabu, nikawaambia: Mukunywe divai. Lakini wao wakajibu: Sisi hatukunywi divai, maana Yonadabu mwana wa Rekabu, babu yetu, alituamuru hivi: Musikunywe divai; musikunywe ninyi wenyewe wala wana wenu milele. Musijenge nyumba, musilime mashamba, wala musikuwe na shamba la mizabibu. Lakini mutaishi katika mahema siku zote za maisha yenu, kusudi mupate kuishi siku nyingi katika inchi munamoishi kama wageni. Sisi tumeitii amri hiyo ya babu yetu Yonadabu mwana wa Rekabu siku zote, juu ya jambo alilotuamuru. Sisi hatukunywi divai hata kidogo; sisi wenyewe hatukunywi, wala wake zetu, wala watoto wetu wanaume au wanawake. Sisi hatujijengei nyumba za kuishi ndani yake. Hatuna mashamba ya mizabibu wala mashamba ya kulima na kupanda mbegu. Sisi tumeishi katika mahema na kutii mambo yote ambayo Yonadabu, babu yetu, alituamuru. Lakini Nebukadneza, mufalme wa Babeli alipofika, kuishambulia inchi hii, tuliamua kuja Yerusalema kwa kuepuka waaskari wa Wakaldea na wa Wasuria. Kwa hiyo sasa tunaishi katika muji Yerusalema. Kisha neno la Yawe lilimufikia Yeremia kusema hivi: Yawe wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi: Kwenda uwaambie watu wa inchi ya Yuda na wakaaji wa Yerusalema hivi: Ninyi hamuwezi kupokea mafundisho na kusikia maneno yangu? –Ni ujumbe wa Yawe! Ile amri ambayo Yonadabu mwana wa Rekabu aliwapa wana wake kwamba wasikunywe divai, imefuatwa; nao hawakunywi divai mpaka siku hii ya leo, maana wametii amri ya babu yao. Lakini mimi nilisema nanyi tena na tena, nanyi hamukunisikiliza. Niliwapelekea tena na tena watumishi wangu wote, ni kusema manabii wawaambie kila mumoja wenu aachane na mwenendo wake mwovu, abadilishe matendo yake na kuacha kuifuata na kuitumikia miungu mingine. Na kwamba mukifanya hivyo mutakaa katika inchi niliyowapa ninyi na babu zenu. Lakini ninyi hamukunitegea sikio wala hamukunisikiliza. Wana wa Yonadabu mwana wa Rekabu wameshika amri waliyopewa na babu yao; lakini ninyi hamukunitii. Kwa hiyo, Yawe wa majeshi, Mungu wa Israeli anasema hivi: Ninawaletea Wayuda na wakaaji wote wa Yerusalema hasara zote nilizosema juu yao, kwa sababu mimi nilisema nao, lakini hawakunisikiliza; niliwaita, lakini hawakuniitikia. Lakini Yeremia aliwaambia Warekabu hivi: Yawe wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi: Ninyi Warekabu mumetii amri ya babu yenu, mukashika kanuni zake zote na kutenda kama alivyowaamuru. Kwa hiyo Yawe wa majeshi anasema hivi: Yonadabu mwana wa Rekabu hatakosa hata mara moja mutu wa uzao wake wa kunitumikia siku zote. Katika mwaka wa ine wa utawala wa mufalme Yoyakimu wa Yuda mwana wa Yosia, ujumbe huu wa Yawe ukatolewa kwa Yeremia: Twaa kizingo cha kitabu uandike humo maneno yote niliyokuambia juu ya Israeli, juu ya Yuda na mataifa yote, tangu siku nilipoanza kusema nawe, wakati Yosia alipokuwa mufalme mpaka leo. Labda watu wa Yuda watasikia juu ya hasara zote ambazo nimekusudia kuwatendea, kusudi kila mumoja wao auache mwenendo wake mubaya, nami nipate kuwasamehe makosa yao na zambi yao. Halafu Yeremia akamwita Baruku mwana wa Neria. Naye Baruku akaandika katika kitabu maneno yote yaliyotoka katika kinywa cha Yeremia sawa vile Yawe alivyokuwa amemwambia. Kisha, Yeremia akamupa Baruku maagizo haya: Mimi siruhusiwi kwenda katika nyumba ya Yawe. Lakini kwa siku ya kwanza ya kufunga kula chakula, wewe utakwenda mbele ya watu wote, ndani ya nyumba ya Yawe, usome kitabu chenye maneno ya Yawe uliyoyaandika kutoka katika kinywa changu. Utayasoma maneno hayo mbele ya watu wote wa Yuda waliofika kutoka miji yao vilevile. Labda maombi yao yatamufikia Yawe na kila mumoja wao ataacha mwenendo wake mubaya kwa maana hasira na kasirani ambavyo Yawe amesema juu ya watu hawa ni kubwa sana. Basi, Baruku mwana wa Neria alitimiza yote aliyoamuriwa na nabii Yeremia juu ya kusoma maneno ya Yawe ndani ya nyumba ya Yawe kutoka katika kitabu hicho. Katika mwaka wa tano wa utawala wa mufalme Yoyakimu wa Yuda mwana wa Yosia, katika mwezi wa kenda, wakaaji wote wa Yerusalema na watu wote waliofika Yerusalema kutoka miji ya Yuda, walitangaza siku ya kufunga kula chakula mbele ya Yawe. Basi, Baruku alisoma maneno ya Yeremia kutoka katika kile kitabu mbele ya watu wote, ndani ya nyumba ya Yawe, katika chumba cha Gemaria mwana wa Safanu aliyekuwa katibu. Chumba hicho kilikuwa katika baraza la juu, kwenye mulango mupya wa nyumba ya Yawe. Mikaya mwana wa Gemaria, mujukuu wa Safanu, aliposikia maneno yote ya Yawe ambayo yalisomwa kutoka kile kitabu, alikwenda kwenye nyumba ya kifalme na kuingia katika chumba cha katibu. Mule mulikuwa wakubwa wote: katibu Elisama, Delaya mwana wa Semaya, Elnatana mwana wa Akibori, Gemaria mwana wa Safanu, Zedekia mwana wa Hanania, na wakubwa wote. Mikaya aliwaambia maneno yote aliyoyasikia wakati Baruku aliposoma kitabu mbele ya watu. Kisha, wakubwa wakamutuma Yehudi mwana wa Netania, mujukuu wa Selemia, kijukuu cha Kusi, amwambie Baruku hivi: Twaa kile kitabu ulichosoma mbele ya watu ukuje nacho hapa. Basi, Baruku mwana wa Neria akatwaa kitabu katika mukono wake, akawaendea. Nao wakamwambia: Ikaa, ukisome. Baruku akawasomea. Waliposikia maneno hayo yote, waliangaliana kwa hofu. Wakamwambia Baruku: Tunapaswa kumwelezea mufalme maneno haya yote. Kisha wakamwuliza Baruku: Basi utuambie, umepata namna gani kuandika maneno haya yote? Yeremia alisema, nawe ukayaandika? Baruku akawajibu: Yeye alisema, nami nikayaandika kwa wino katika kitabu hiki. Kisha wakubwa hao wakamwambia Baruku: Wewe uende ujifiche pamoja na Yeremia, na kusikuwe mutu yeyote atakayejua pahali munapokuwa. Wale wakubwa walipokwisha kuweka kitabu kile katika chumba cha Elisama katibu wa mufalme, walimwendea mufalme ndani ya kiwanja, wakamujulisha mambo yote. Kisha, mufalme alimutuma Yehudi aende kuleta kile kitabu. Yehudi alikitwaa kutoka ndani ya chumba cha katibu Elisama, akamusomea mufalme na wakubwa wote waliokuwa wamesimama karibu na mufalme. Wakati huo ulikuwa mwezi wa kenda, na mufalme alikuwa ndani ya nyumba yake ya nyakati za baridi. Mbele yake kulikuwa moto wa makaa. Yehudi alipokuwa amekwisha kusoma vipindi vitatu au vine hivi vya kitabu kile, mufalme alivikatakata kwa kisu na kuvitupa katika moto wa makaa. Aliendelea kufanya hivyo mpaka kitabu chote kikateketezwa. Lakini, ingawa mufalme na watumishi wake wote waliyasikia maneno hayo yote, hawakuogopa wala kurarua nguo zao kwa huzuni. Ijapokuwa Elnatana, Delaya na Gemaria walimusihi mufalme asikichome kile kitabu, mufalme hakuwasikiliza. Mufalme alimwamuru mwana wake Yerameli, Seraya mwana wa Azirieli na Selemia mwana wa Abudieli, wamukamate katibu Baruku na nabii Yeremia. Lakini Yawe aliwaficha. Mufalme alipokwisha kuchoma kwa moto kile kitabu ambacho Baruku aliandika kwa maagizo ya Yeremia, neno la Yawe lilimufikia Yeremia kusema hivi: Twaa kitabu kingine, uandike maneno yote yaliyokuwa katika kile cha kwanza ambacho Yoyakimu, mufalme wa Yuda, amechoma kwa moto. Nawe utamwambia huyo Yoyakimu mufalme wa Yuda kwamba: Yawe anasema hivi: Umekichoma kwa moto kitabu hicho na kuuliza kwa nini Yeremia ameandika kwamba mufalme wa Babeli atakuja kuiharibu inchi hii na kuwaangamiza watu na nyama! Basi, Yawe anasema hivi juu yake yeye Yoyakimu mufalme wa Yuda: Yeye hatakuwa na mutu wa uzao wake atakayeikalia kiti cha kifalme cha Daudi, na maiti yake itatupwa inje kwenye joto muchana na baridi kali usiku. Nami nitamwazibu yeye na wazao wake pamoja na watumishi wake kwa sababu ya uovu wao. Nitawaletea wao na wakaaji wote wa Yerusalema pamoja na watu wote wa Yuda hasara yote niliyosema juu yao na ambayo hawakuijali. Kisha, Yeremia alitwaa kitabu kingine, akamupa katibu Baruku mwana wa Neria, ambaye aliandika humo maneno yote aliyoambiwa na Yeremia ambayo yalikuwa katika kile kitabu cha mbele ambacho Yoyakimu, mufalme wa Yuda, alichoma kwa moto. Maneno mengine ya namna hiyo yaliongezwa. Mufalme Nebukadneza wa Babeli alimusimika Zedekia mwana wa Yosia kuwa mufalme wa Yuda pahali pa Konia mwana wa Yoyakimu. Lakini Zedekia na wakubwa wake pamoja na wanainchi wa Yuda hawakusikiliza maonyo Yawe aliyotoa kwa njia ya nabii Yeremia. Mufalme Zedekia aliwatuma Yehukali mwana wa Selemia, pamoja na kuhani Zefania mwana wa Maseya, kwa nabii Yeremia kusema awaombee kwa Yawe, Mungu wao. Wakati huo, Yeremia alikuwa angali na uhuru wa kutembea kati ya watu, maana alikuwa hajatiwa katika kifungo. Tena waaskari wa mufalme wa Misri walikuwa wameondoka Misri, na waaskari wa Wakaldea walikuwa wameuzunguka Yerusalema waliposikia habari hizo waliondoka. Halafu neno la Yawe lilimufikia Yeremia kusema hivi: Yawe, Mungu wa Israeli, anasema hivi: Utamwambia mufalme wa Yuda hivi ambaye amekutuma uniombe kwa ajili yake: Waaskari wa Mufalme wa Misri waliokuja kukusaidia, wako karibu kurudia kwao Misri. Na Wakaldea watarudi kuushambulia muji huu. Watauteka muji na kuuteketeza kwa moto. Yawe anasema hivi: Musijidanganye wenyewe na kusema kwamba waaskari wa Wakaldea wataondoka. Kweli hawataondoka. Hata kama mukiwashinda waaskari wote wa Wakaldea wanaopigana nanyi na kunabaki tu katika mahema yao wale walioumizwa, hao watasimama na kuuteketeza muji huu kwa moto. Kundi la waaskari wa Wakaldea lilipoondoka Yerusalema kwa kulikimbia kundi la waaskari wa mufalme wa Misri lililokuwa linakaribia, Yeremia aliondoka Yerusalema kwenda katika inchi ya Benjamina kwa kupokea sehemu ya urizi wake. Alipokuwa katika mulango wa Benjamina, mulinzi mumoja anayeitwa Iria mwana wa Selemia, mujukuu wa Hanania, alimukamata Yeremia na kumwambia: Wewe unatoroka kusudi uende kujiunga na Wakaldea! Yeremia akamwambia: Huo ni uongo! Mimi sitoroki na kwenda kujiunga na Wakaldea. Lakini Iria hakusadiki maneno ya Yeremia. Basi akamutia katika kifungo na kumupeleka kwa wakubwa. Wakubwa hao walimukasirikia sana Yeremia wakamupiga, kisha wakamufunga katika kifungo katika nyumba ya katibu Yonatani iliyokuwa imegeuzwa kuwa gereza. Yeremia alipokuwa amefungwa katika gereza kwa muda wa siku nyingi, mufalme Zedekia alimwita na kumukaribisha kwake. Mufalme akamwuliza kwa siri wakiwa katika nyumba yake: Kuna neno lolote kutoka kwa Yawe? Yeremia akamujibu: Ndiyo, kuko. Kisha akaendelea kusema: Wewe utatiwa katika mikono ya mufalme wa Babeli. Halafu Yeremia akamwuliza mufalme Zedekia: Nimekukosea nini, au nimewakosea nini watumishi wako au watu hawa, hata unitie katika kifungo? Wako wapi manabii waliokutabiria wakisema: Mufalme wa Babeli hatakushambulia wewe wala inchi hii? Sasa ninakuomba unisikilize, ee bwana wangu mufalme. Ninakusihi sana ulikubali ombi langu. Tafazali usinirudishe tena katika kifungo katika nyumba ya katibu Yonatani, nisipate kukufia humo. Basi, mufalme Zedekia akatoa amri Yeremia awekwe katika chumba cha walinzi na kupewa mukate kila siku kutoka kwa wapikaji wa mukate mpaka mikate ilipotoweka kabisa huko katika muji. Basi, Yeremia alibaki katika chumba cha walinzi. Sefatia mwana wa Matani, Gedalia mwana wa Pashuri, na Yukali mwana wa Selemia, pamoja na Pushuri mwana wa Malkia walisikia maneno ambayo Yeremia aliwatangazia watu wote akisema: Yawe anasema hivi: Yeyote atakayebaki katika muji huu atakufa kwa vita, njaa na ugonjwa mukali; lakini yule atakayeondoka na kujitoa kwa Wakaldea, ataishi. Maisha yake yatatekwa naye ataishi. Yawe anasema hivi: Hakika muji huu utatiwa katika mikono ya waaskari wa mufalme wa Babeli na kutekwa. Wakubwa wakamwambia mufalme: Inafaa mutu huyu auawe kwa maana anawavunja moyo waaskari ambao wameachwa katika muji huu na watu wote kwa jumla, kwa kusema maneno kama hayo. Yeye hawatakii watu hawa mema lakini mabaya. Mufalme Zedekia akasema: Basi! Mutu huyu yuko katika mikono yenu; mimi siwezi kuwapinga. Basi, wakamutwaa Yeremia wakamutia katika kisima cha Malkia mwana wa mufalme ambacho kilikuwa katika kiwanja cha walinzi. Walimushusha Yeremia ndani kwa kamba. Ndani ya kisima hicho hamukukuwa maji lakini matope, naye Yeremia akazama katika matope. Lakini Ebedimeleki, towashi Mwetiopia aliyetumika katika nyumba ya kifalme, alipata habari kwamba walikuwa wamemutia Yeremia katika kisima. Wakati huo mufalme alikuwa anafanya baraza kwenye mulango wa Benjamina. Basi, Ebedimeleki akamwendea mufalme, akamwambia: Bwana wangu mufalme, watu hawa wamefanya kitu kibaya. Wamemutia yule nabii Yeremia katika kisima ambamo kwa kweli atakufa kwa njaa, kwa maana hakuna chakula tena katika muji. Halafu mufalme akamwamuru yule Mwetiopia Ebedimeleki hivi: Twaa watu watatu kutoka hapa uende umutoe nabii Yeremia katika kisima, mbele hajakufa. Basi, Ebedimeleki akatwaa watu hao na kwenda pamoja nao katika nyumba ya kifalme, wakaingia katika gala ya nyumba ya kifalme; Ebedimeleki akatwaa nguo zilizopasukapasuka na kuchakaa, akaziteremushia Yeremia ndani ya kisima kwa kamba. Kisha yule Mwetiopia Ebedimeleki akamwambia Yeremia: Weka nguo hizo katika makwapa yako, kisha upitishe kamba hizo chini ya nguo hizo. Yeremia akafanya hivyo. Kisha wakamukokota Yeremia kwa kamba, wakamutosha ndani ya kisima. Kisha hayo, Yeremia akaendelea kukaa katika chumba cha walinzi. Wakati fulani mufalme Zedekia alitaka kumwona nabii Yeremia. Basi, akaagiza Yeremia aletwe kwenye mulango wa tatu wa nyumba ya Yawe. Huko, mufalme alimwambia Yeremia: Ninataka kukuuliza jambo fulani; usinifiche kitu chochote. Yeremia akamujibu Zedekia: Nikikuambia ukweli hautaniua? Na kama nikikushauria, hautanisikiliza. Halafu, mufalme Zedekia alimwapia Yeremia kwa siri akisema: Kama vile Yawe, yule aliyetupatia uzima, anavyoishi, sitakuua wala sitakutia katika mikono ya hawa wanaotaka kukuua. Hapo Yeremia akamwambia Zedekia: Yawe wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi: Kama ukijitoa mwenyewe na kujitia katika mikono ya wakubwa wa mufalme wa Babeli, utayaokoa maisha yako na muji hautateketezwa kwa moto; nawe pamoja na jamaa yako mutaendelea kuishi. Lakini usipojitoa mwenyewe na kujitia katika mikono ya wakubwa wa mufalme wa Babeli, basi, muji huu utatekwa na Wakaldea nao watauteketeza kwa moto, nawe hautaweza kujiepusha toka katika mikono yao. Mufalme Zedekia akamwambia Yeremia: Ninawaogopa Wayuda waliokimbilia kwa Wakaldea. Labda nitatolewa kwao, wanitese. Yeremia akamujibu: Hautatolewa kwao. Wewe sasa utii kile Yawe anachosema, kama ninavyokuambia, na mambo yote yatakuendekea vema, na maisha yako yataokolewa. Lakini kama ukikataa kujitoa mwenyewe na kujitia katika mikono yao, haya ndiyo maono ambayo Yawe amenionyesha. Katika maono hayo, niliona wanawake waliobaki katika nyumba ya kifalme ya mufalme wa Yuda wakipelekwa kwa wakubwa wa mufalme wa Babeli, nao walikuwa wakisema hivi: Warafiki zako uliowaaminia wamekudanganya, nao wamekushinda. Miguu yako imezama ndani ya matope, nao wanakugeuka na kukuacha. Wake wako wote na watoto wako watapelekwa kwa Wakaldea, nawe mwenyewe hautaponyoka. Utakamatwa mateka na mufalme wa Babeli na muji huu utateketezwa kwa moto. Zedekia akamwambia Yeremia: Mutu yeyote asijue habari hizi, nawe hautauawa. Kama wakubwa wakisikia kwamba nimeongea nawe, kisha wakikuja na kukuambia: Basi utuambie, ulizungumuza nini na mufalme. Usitufiche chochote nasi hatutakuua; wewe utawaambia hivi: Nilikuwa ninamusihi mufalme kwa unyenyekevu asinirudishe katika kifungo ndani ya nyumba ya Yonatani, nisikuje kukufia huko. Kisha, wakubwa walimufikia Yeremia wakamwuliza mambo hayo, naye akawajibu kama vile mufalme alivyomwelekeza. Halafu waliacha kuzungumuza naye kwa sababu hakuna mutu aliyekuwa amesikia mazungumuzo yake na mufalme. Yeremia alibaki katika chumba cha walinzi mpaka siku muji Yerusalema ulipotekwa. Katika mwezi wa kenda wa mwaka wa kenda wa utawala wa Zedekia mufalme wa Yuda, Nebukadneza mufalme wa Babeli alifika na waaskari wake wote kuushambulia Yerusalema, akauzunguka kwa vita. Na katika siku ya kenda ya mwezi wa ine, mwaka wa kumi na moja wa utawala wa Zedekia, sehemu ya ukuta wa muji ilibomolewa. (Basi wakubwa hawa wote wa mufalme wa Babeli waliingia na kukaa kwenye mulango wa katikati: Nergali-Sarezeri, Samgari-Nebo, Sarsekimu jemadari mukubwa wa na Nergali-Sarezeri mukubwa wenye maarifa, pamoja na wakubwa wengine wote wa mufalme wa Babeli.) Naye Zedekia, mufalme wa Yuda na waaskari wake wote walipowaona, walitoroka. Walitoka inje ya muji usiku, wakipitia katika bustani ya mufalme, kwenye mulango katikati ya kuta mbili, wakatelemukia kwenye bonde la muto Yordani. Lakini kundi la waaskari la Wakaldea liliwafuatilia na kumukamata Zedekia karibu na Yeriko. Kisha kumukamata walimufikisha kwa Nebukadneza, mufalme wa Babeli huko Ribla, katika inchi ya Hamati, naye akamuhukumu. Kulekule Ribla, mufalme wa Babeli aliwaua wana wa Zedekia mbele ya baba yao. Waliwaua vilevile wakubwa wote wa Yuda. Kisha aliongoa macho ya Zedekia na kumufunga kwa minyororo, kusudi amupeleke Babeli. Wakaldea waliichoma kwa moto nyumba ya kifalme na nyumba za watu; vilevile walizibomoa kuta za Yerusalema. Kisha, Nebuzaradani, mukubwa wa walinzi wa mufalme, aliwapeleka katika uhamisho kule Babeli watu waliokuwa wamebaki katika muji na wale waliokuwa wamejitoa kwake pamoja na wafundi wote waliokuwa wamebaki. Nebuzaradani, mukubwa wa walinzi wa mufalme, aliwaacha katika inchi ya Yuda watu wamoja wamasikini ambao hawakukuwa na kitu chochote, akawagawanyia mashamba ya mizabibu na kuwapa maeneo ya kulima wakati huohuo. Nebukadneza mufalme wa Babeli alikuwa amemupa Nebuzaradani mukubwa wa walinzi, amri hii juu ya Yeremia: Umutwae Yeremia, umutunze vema wala usimuzuru; umutendee kama anavyokuambia. Basi, Nebuzaradani mukubwa wa walinzi, Nebusazibani, Nergali-Sarezeri pamoja na wakubwa wote wa mufalme wa Babeli, wakatuma watu wamwondoe Yeremia katika chumba cha walinzi. Wakamutoa Yeremia kwa Gedalia mwana wa Ahikamu, mujukuu wa Safanu, amupeleke katika nyumba yake. Basi, Yeremia akaishi pamoja na wanainchi wengine. Wakati Yeremia alipokuwa amefungwa katika chumba cha walinzi, neno la Yawe lilimufikia kusema hivi: Kwenda kwa Ebedimeleki Mwetiopia umwambie hivi: Yawe wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi: Angalia mimi nitatimiza mambo yale niliyosema juu ya muji huo na sio mambo mema. Mambo hayo yatakamilika siku hiyo ukiona wewe mwenyewe. Lakini siku hiyo mimi nitakuokoa wewe, wala hautatiwa katika mikono ya watu unaowaogopa. Maana, kweli nitakuokoa na hautauawa kwa vita; utapata faida ya kuokoa maisha yako kwa sababu umeniamini mimi. –Ni ujumbe wa Yawe. Huu ni ujumbe uliotolewa kwa Yeremia kutoka kwa Yawe wakati Nebuzaradani mukubwa wa walinzi wa mufalme alipomuruhusu Yeremia aondoke Rama. Huyo mukubwa alimukamata Yeremia akifungwa minyororo, pamoja na wafungwa wengine wote wa Yerusalema na Yuda ambao walikuwa wamepelekwa katika uhamisho kule Babeli. Mukubwa wa walinzi alimukamata Yeremia, akamwambia: Yawe, Mungu wako, alitangaza hasara juu ya pahali hapa. Na sasa Yawe ametimiza jambo hilo na kutenda kama alivyosema. Kwa sababu ninyi wote mulimukosea Yawe na kukataa kumutii, jambo hilo limewapata. Basi! Leo ninafungua minyororo toka mikono yako. Kama unaona ni vizuri kwenda pamoja nami mpaka Babeli, basi tuende pamoja; mimi nitakutunza vizuri. Lakini kama unaona si vizuri kwako kwenda pamoja nami mpaka Babeli, basi, usikuje. Ujue kwamba unaweza kwenda popote katika inchi hii. Basi kwenda kwenye unaona ni vizuri kwenda. Kama ukiamua kubaki, basi rudi kwa Gedalia mwana wa Ahikamu, mujukuu wa Safanu, ambaye mufalme wa Babeli amemusimika kuwa mutawala wa miji yote ya Yuda, ukae naye kati ya wanainchi wengine. Kama sivyo, kwenda kwenye unaona unastahili kwenda. Basi, mukubwa wa walinzi akamupa Yeremia vyakula na zawadi, kisha akamwacha ajiendee. Kisha Yeremia akaenda Misipa kwa Gedalia mwana wa Ahikamu, akakaa naye pamoja na wanainchi waliobaki katika inchi. Wakubwa wote wa waaskari kutoka katika pori pamoja na watu wao, waliposikia kwamba mufalme wa Babeli alikuwa amemusimika Gedalia mwana wa Ahikamu, kuwa mutawala wa inchi, na kwamba alikuwa amewaweka chini ya usimamizi wake wanaume, wanawake na watoto, ni kusema watu wakosefu kabisa katika inchi ambao hawakupelekwa katika uhamisho kule Babeli, walimwendea Gedalia kule Misipa. Watu hao walikuwa Isimaeli mwana wa Netania, Yohana na Yonatani wana wa Karea, Seraya mwana wa Tanumeti, nao wana wa Efai kutoka muji Netofa, na Yezania wa muji wa Makati; wote pamoja na watu wao. Gedalia aliapa mbele yao na mbele ya waaskari wao akisema: Musiogope kuwatumikia Wakaldea. Mukae katika inchi mumutumikie mufalme wa Babeli, na mambo yote yatawaendekea vema. Mimi nitakaa Misipa nipate kuwa musimamizi wenu mbele ya Wakaldea watakaofika kwetu; lakini ninyi muvune matunda na mukamue divai na mafuta, mujiwekee akiba ya vitu hivyo, mukae katika miji mutakayoirizi. Vilevile Wayuda waliokuwa katika inchi ya Moabu na kati ya Waamoni na katika inchi ya Edomu na inchi zingine, waliposikia kwamba mufalme wa Babeli amewaruhusu Wayuda wengine kubaki katika inchi ya Yuda na kwamba amemusimika Gedalia mwana wa Ahikamu, mujukuu wa Safanu kuwa mutawala wao, wote walirudi kutoka pahali pote walipokuwa wametawanyika na kwenda katika inchi ya Yuda kwa Gedalia kule Misipa. Walichuma zabibu na matunda mengine kwa wingi sana. Basi, Yohana mwana wa Karea pamoja na wakubwa wote wa waaskari kutoka katika pori, walifika kwa Gedalia, kule Misipa, wakamwambia: Uko na habari kwamba Balisi mufalme wa Waamoni, amemutuma Isimaeli mwana wa Netania, akuue? Lakini Gedalia mwana wa Ahikamu hakuamini maneno yao. Kisha, Yohana mwana wa Karea akazungumuza na Gedalia kwa siri kule Misipa, akamwambia: Uniruhusu niende nimwue Isimaeli mwana wa Netania, na hakuna mutu yeyote atakayejua. Kwa nini kumwachilia yeye akuue na Wayuda wote waliokusanyika hapa watawanyike na Wayuda waliobaki waangamie? Lakini Gedalia mwana wa Ahikamu akamwambia Yohana mwana wa Karea hivi: Usifanye jambo hilo! Mambo unayosema juu ya Isimaeli si ya kweli! Katika mwezi wa saba, Isimaeli mwana wa Netania, mujukuu wa Elisama, wa ukoo wa kifalme, mumoja wa wasimamizi wa mufalme alifika Misipa kwa Gedalia pamoja na watu kumi. Wakati walipokuwa wakikula chakula kule Misipa, Isimaeli mwana wa Netania pamoja na wale watu kumi, wakasimama na kumushambulia kwa upanga Gedalia mwana wa Ahikamu, mujukuu wa Safanu, wakamwua. Gedalia ndiye aliyekuwa amesimikwa na mufalme wa Babeli kuwa mutawala wa inchi. Isimaeli aliwaua vilevile Wayuda wote waliokuwa pamoja na Gedalia huko Misipa na waaskari Wakaldea waliokuwa pahali pale. Siku moja kisha kumwua Gedalia, mbele hata mutu yeyote hajajua habari hizo, kulifika watu makumi nane kutoka Sekemu, Shilo na Samaria. Walikuwa wamenyoa ndevu zao na wamevaa nguo zilizotatuka na miili yao imechanjwachanjwa. Walileta sadaka ya ngano na ubani vitolewe katika nyumba ya Yawe. Isimaeli mwana wa Netania, alitoka inje ya muji kukutana na watu hao akiwa analia. Alipokutana nao, akawaambia: Karibu ndani ya nyumba kwa Gedalia mwana wa Ahikamu. Walipoingia katika muji, Isimaeli mwana wa Netania, pamoja na wale watu kumi waliokuwa pamoja naye, waliwaua watu hao na kuzitupa maiti zao ndani ya kisima. Lakini kulikuwa watu kumi katika kundi hilo waliomwambia Isimaeli hivi: Tafazali usituue, maana tuna akiba kubwa ya ngano, shayiri, mafuta na asali ambayo tumeificha katika pori. Basi hao akawaacha wazima. Kisima ambamo Isimaeli alitupa maiti za wale watu aliowaua ni kile kikubwa ambacho mufalme Asa alikuwa amekichimba kwa kujikinga na Basha, mufalme wa Waisraeli. Isimaeli mwana wa Netania alikijaza kisima hicho maiti za wale watu aliowaua. Kisha, Isimaeli aliwakamata wabinti wa mufalme mateka na watu wote waliobaki kule Misipa, watu ambao Nebuzaradani, mukubwa wa walinzi, alikuwa amewaweka chini ya ulinzi wa Gedalia mwana wa Ahikamu. Isimaeli mwana wa Netania, aliwakamata mateka hao, akaondoka, akaenda kwa Waamoni. Lakini Yohana mwana wa Karea, pamoja na wakubwa wote wa waaskari, waliposikia juu ya uovu ambao Isimaeli mwana wa Netania, alikuwa ameufanya, waliwakusanya watu wao wote, wakaenda kupigana na Isimaeli. Walimukuta kwenye kisima kikubwa cha Gibeoni. Watu wote waliotekwa na Isimaeli walipomwona Yohana mwana wa Karea, pamoja na wakubwa wote wa waaskari, walifurahi sana. Basi, watu hao wote ambao Isimaeli alikuwa amewakamata mateka kutoka Misipa, waligeuka, wakarudi nyuma, wakamwendea Yohana mwana wa Karea. Lakini Isimaeli mwana wa Netania, pamoja na watu wanane waliponyoka kutoka kwa Yohana, wakakimbilia kwa Waamoni. Kisha, Yohana mwana wa Karea pamoja na wakubwa wote wa waaskari waliokuwa pamoja naye, waliwakamata watu wote waliobaki, ambao Isimaeli mwana wa Netania, alikuwa amewakamata mateka kutoka Misipa kisha kumwua Gedalia mwana wa Ahikamu, ni kusema: waaskari, wanawake, watoto na matowashi wa nyumba ya mufalme. Yohana aliwarudisha wote kutoka Gibeoni. Basi, wakajiendea, wakakaa huko Geruti–Kimuhamu karibu na Betelehemu. Wakikusudia kuingia katika inchi ya Misri, kwa sababu walikuwa wanawaogopa Wakaldea tangu wakati Isimaeli mwana wa Netania, alipomwua Gedalia mwana wa Ahikamu ambaye mufalme wa Babeli alikuwa amemusimika kuwa mutawala wa inchi. Kisha wakubwa wote wa waaskari, Yohanani mwana wa Karea, na Azaria mwana wa Hosaya pamoja na watu wote, wadogo kama vile wakubwa, wakamwendea Yeremia, wakamwambia: Tafazali sikiliza maombi yetu na kutuombea kwa Yawe, Mungu wako, sisi wote tuliobaki, kwa maana tulikuwa wengi, lakini sasa tumebaki wachache tu, kama unavyoona. Yawe, Mungu wako, atuonyeshe njia anayotaka tuifuate, na kile anachotaka tufanye. Yeremia akawajibu: Vema; nimesikia. Nitamwomba Yawe, Mungu wenu, kama mulivyonisihi; jibu lolote Yawe atakalonipa, nitawaambia; sitawaficha kitu chochote. Kisha, watu wakamwambia Yeremia: Yawe akuwe mushuhuda wa kweli na mwaminifu juu yetu ikiwa hatutafanya jinsi Yawe, Mungu wako atakavyokuagiza utuambie. Ikuwe ni jambo la kupendeza au hapana, sisi tutaitii sauti ya Yawe, Mungu wetu, ambaye tunakutuma kwake kusudi mambo yatuendekee vizuri tutakapomutii Yawe, Mungu wetu. Nyuma ya siku kumi, neno la Yawe lilimufikia Yeremia. Basi, Yeremia akamwita Yohana mwana wa Karea, na wakubwa wote wa waaskari pamoja na watu wote, wadogo kama vile wakubwa, akawaambia: Yawe, Mungu wa Israeli, ambaye ninyi mulinituma kwake nipeleke maombi yenu, anasema hivi: Kama ninyi mutabaki katika inchi hii, basi, nitawasimamisha, wala sitawaharibu; nitawaotesha wala sitawaongoa; kwa maana nitabadilisha nia kwa sababu ya hasara niliyowatendea. Musimwogope mufalme wa Babeli munayemwogopa; musimwogope hata kidogo. Mimi niko pamoja nanyi kwa kuwaokoa na kuwaponyesha kutoka katika mikono yake. Nitawahurumia na kumufanya mufalme awahurumie na kuwaacha katika inchi yenu. –Ni ujumbe wa Yawe. Lakini mukisema: Hatutaki kubaki katika inchi hii, na hivyo mukiacha kutii sauti ya Yawe, Mungu wenu, na kusema kwamba mutakwenda kukaa katika inchi ya Misri, ambako hamutaona vita wala kusikia sauti ya baragumu wala kukosa chakula, basi, musikilize jinsi Yawe anavyosema enyi mabaki ya Yuda. Yawe, Mungu wa Israeli, anasema hivi: Kama mumekusudia kwenda katika inchi ya Misri na kukaa huko, basi, vita munavyoviogopa vitawakuta kulekule Misri, na njaa munayoogopa itawaandama vikali mpaka Misri, na mutakufia kulekule. Watu wote wenye nia ya kwenda kukaa Misri watakufa kwa njaa na ugonjwa mukali wala hakuna hata mumoja wao atakayebaki au kuponyoka kutokana na hasara nitakayowaletea. Maana Yawe wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi: Kama vile hasira yangu na kasirani yangu ilivyowapata wakaaji wa Yerusalema, ndivyo kasirani yangu itakavyowapata ninyi, kama mutakwenda Misri. Mutakuwa kitu cha kutukaniwa, kitisho, laana na haya. Hamutaona tena nafasi hii. Yeremia akawaambia watu: Enyi Wayuda muliobaki, Yawe aliwaambia musiende Misri. Mujue wazi kwamba leo nimewaonya kwamba mumepotoka, mumeyahatarisha maisha yenu. Maana mulinituma kwa Yawe, Mungu wenu, mukiniambia: Utuombee kwa Yawe, Mungu wetu kwamba kitu chochote Yawe, Mungu wetu, atakachosema, utuambie, nasi tutatimiza. Leo mimi nimewaambia, lakini hamukutii neno lolote ambalo Yawe, Mungu wenu amenituma niwaambie. Basi, mujue hakika kwamba mutauawa kwa vita, kwa njaa na kwa ugonjwa mukali katika inchi ile munayotaka kwenda kukaa ndani yake. Yeremia alipomaliza kuwaambia watu wote maneno yote ambayo Yawe, Mungu wao, alimwamuru awatangazie, Azaria mwana wa Hosaya, Yohana mwana wa Karea na watu wote wenye kiburi, walimwambia Yeremia: Yawe, Mungu wetu, hakukutuma wewe utuambie tusiende Misri, tuishi huko. Baruku mwana wa Neria, amekuchochea juu yetu kusudi tutiwe katika mikono ya Wakaldea watuue au watupeleke katika uhamisho kule Babeli. Basi, Yohana mwana wa Karea na wakubwa wote wa waaskari pamoja na watu wote hawakutii maneno ya Yawe, kwamba wabaki katika inchi ya Yuda. Halafu Yohana mwana wa Karea na wakubwa wote wa waaskari waliwapeleka watu wote wa Yuda waliobaki ambao walikuwa wamerudi katika inchi ya Yuda kutoka katika mataifa yote ambako walikuwa wamesambazwa: wanaume, wanawake, watoto, wabinti wa mufalme na kila mutu ambaye Nebuzaradani mukubwa wa waaskari alikuwa amemwachia Gedalia mwana wa Ahikamu mujukuu wa Safanu. Wakamupeleka vilevile nabii Yeremia na Baruku mwana wa Neria. Wakaenda katika inchi ya Misri, wakafika katika muji wa Tapanesi. Ndivyo walivyokataa kutii maneno ya Yawe. Wakati Yeremia alipokuwa Tapanesi, neno la Yawe lilimufikia Yeremia kusema hivi: Twaa mawe makubwa, uyafiche ndani ya udongo kwenye matofali mbele ya mulango wa nyumba ya kifalme ya Tapanesi mbele ya Wayuda. Kisha uwaambie hivi: Yawe, Mungu wa Israeli, anasema hivi: Muangalie, mimi nitamutuma na kumuleta Nebukadneza, mufalme wa Babeli, mutumishi wangu, naye ataweka kiti chake cha kifalme juu ya mawe haya ambayo nimeyaficha hapa, na kutandaza paa la kifalme juu yake. Atakapofika ataiangamiza inchi ya Misri. Kwa hiyo waliopangiwa kufa kwa ugonjwa watakufa kwa ugonjwa, waliopangiwa kukamatwa mateka, watakamatwa mateka; waliopangiwa kufa kwa vita watakufia katika vita. Mimi nitawasha moto katika mahekalu ya miungu ya Misri; naye Nebukadneza ataiteketeza miungu hiyo kwa moto au kuikamata mateka mpaka Babeli. Ataisafisha inchi ya Misri kama muchungaji anavyoondoa vidudu katika nguo yake na kuondoka Misri akiwa mushindi. Ataivunja minara ya mungu wao inayokuwa huko Heliopoli katika inchi ya Misri, na atateketeza mahekalu ya miungu ya Misri kwa moto. Yawe akamutolea Yeremia ujumbe juu ya Wayuda waliokuwa wanakaa katika inchi ya Misri katika miji ya Migidoli, Tapanesi, Nofi na sehemu ya Patro: Yawe wa majeshi, Mungu wa Israeli anasema hivi: Ninyi mumeona hasara yote niliyouletea Yerusalema na miji yote ya Yuda. Miji hii ni mabomoko mpaka leo wala hakuna mutu anayeishi humo. Imekuwa hivyo kwa sababu ya uovu walioufanya, wakanikasirikisha kwa kuifukizia ubani na kuitumikia miungu mingine ambayo wao wenyewe hawakuifahamu, wala ninyi, wala babu zenu. Hata hivyo, mimi niliwatuma kwenu siku zote watumishi wangu manabii nikisema: Musifanye jambo hili baya ninalolichukia! Lakini hakuna aliyenisikiliza wala kunitegea sikio. Ninyi mulikataa kuacha uovu wenu na kuacha kuifukizia miungu mingine ubani. Kwa hiyo, kasirani yangu na hasira yangu iliwaka na kumwangika juu ya miji ya Yuda na barabara za Yerusalema, hata kukakuwa jangwa na mabomoko kama inavyokuwa mpaka leo. Sasa, Yawe wa majeshi, Mungu wa Israeli anasema hivi: Mbona munajiletea maovu makubwa namna hii, na kujiangamiza ninyi wenyewe, wanaume kama vile wanawake, watoto wadogo na wachanga, hata kusibaki mutu katika inchi ya Yuda? Kwa nini munanichochea nikasirike kwa kuabudu sanamu mulizojitengenezea wenyewe na kuifukizia ubani miungu mingine katika inchi ya Misri ambamo mumekuja kuishi? Munataka kuangamizwa na kuwa laana na kuchekelewa mbele ya mataifa yote katika dunia? Mumesahau uovu wa babu zenu, uovu wa wafalme wa Yuda, uovu wa wake wao na uovu wenu ninyi wenyewe na wa wake wenu, ambao muliufanya katika inchi ya Yuda na kwenye barabara za Yerusalema? Mpaka hivi leo hamujajinyenyekeza wala kuogopa wala kuzifuata sheria zangu na masharti yangu nilizowawekea ninyi na babu zenu. Kwa hiyo, Yawe wa majeshi, Mungu wa Israeli anasema hivi: Basi, nitawageukia na kuwaletea hasara na kuiangamiza Yuda yote. Nitawaondoa Wayuda waliobaki ambao wanaokazania kwenda kukaa Misri, na kuwaangamiza wote, wakubwa kama vile wadogo; watakufa kwa upanga au kwa njaa. Watakuwa takataka, kitu cha kutisha, cha laana na kuchekelewa. Nitawaazibu wale wanaokaa katika inchi ya Misri kama nilivyouazibu Yerusalema, kwa vita, njaa, na ugonjwa mukali. Kwa hiyo hakutakuwa mutu hata mumoja kati ya watu wa Yuda waliobaki na kwenda kukaa katika inchi ya Misri ambaye ataponyoka au kuishi au kurudi katika inchi ya Yuda ambayo wanatamani kurudi na kuishi humo. Hawatarudi, isipokuwa tu wakimbizi wachache. Kisha, wanaume wote waliojua kwamba wake wao walikuwa wameifukizia miungu mingine ubani, na wanawake wote waliokuwa hapo, kusanyiko kubwa la watu pamoja na Waisraeli waliokuwa wanakaa Patro katika inchi ya Misri walimujibu Yeremia: Juu ya neno ulilotuambia kwa jina la Yawe, hatutakusikiliza. Lakini kila kitu tulichoapa kufanya tutafanya: Tutamufukizia ubani malkia wa mbinguni na kumutolea sadaka ya kinywaji kama tulivyokuwa tunafanya sisi wenyewe na babu zetu, wafalme wetu na wakubwa wetu, katika miji ya Yuda na katika barabara za Yerusalema. Kwa wakati huo tulikuwa na chakula tele, tulistawi na hatukuona hasara yoyote. Lakini tangu tulipoacha kumufukizia malkia wa mbinguni ubani na sadaka ya kinywaji, tumekosewa kila kitu, na tumeangamizwa kwa vita na njaa. Nao wanawake wakasema: Tulimufukizia malkia wa mbinguni ubani na kumutolea sadaka ya kinywaji. Tulifanya hivyo kwa ruhusa ya waume wetu. Tena tulimutengenezea mikate yenye sura yake na kumutolea sadaka ya kinywaji. Halafu Yeremia akawaambia watu wote, wanaume na wanawake, ni kusema watu wote waliomupa jibu hilo: Juu ya matambiko ambayo ninyi na babu zenu, wafalme wenu na wakubwa wenu, pamoja na wanainchi wote, mulitoa katika miji ya Yuda na katika barabara za Yerusalema, munazani Yawe amesahau au hakumbuki? Yawe hakuweza kuvumilia tena matendo yenu maovu na mambo ya kuchukiza muliyotenda; ndiyo maana inchi yenu imekuwa ukiwa, jangwa, laana na bila wakaaji, kama inavyokuwa mpaka leo. Hasara hizi zimewapata mpaka leo kwa sababu muliitolea miungu mingine sadaka za kuteketezwa na kumukosea Yawe, mukakataa kusikiliza sauti yake au kufuata sheria yake, masharti yake na maagizo yake. Yeremia aliwaambia watu wote na wanawake wote: Musikilize neno la Yawe, enyi Wayuda wote munaokuwa katika inchi ya Misri. Yawe wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi: Ninyi pamoja na wake wenu mumetimiza kwa vitendo yale muliyosema kwa vinywa vyenu, mukisema kwamba mumekusudia kutimiza viapo vyenu mulivyofanya vya kumutolea malkia wa mbinguni ubani na kumutolea sadaka ya kinywaji. Basi mushike viapo vyenu na kutoa sadaka za vinywaji! Lakini musikilize neno la Yawe, enyi watu wote wa Yuda munaokaa katika inchi ya Misri. Yawe anasema hivi: Ninaapa kwa jina langu kubwa kwamba hakuna mutu yeyote wa Yuda katika inchi yote ya Misri atakayelitumia jina langu kwa kuapa nalo akisema: Kama vile Bwana wangu Yawe anavyoishi. Mimi ninawachungulia hao si kwa mema lakini kwa mabaya. Watu wote wa Yuda katika inchi ya Misri wataangamizwa kwa upanga na njaa, hakutabaki hata mutu mumoja. Ni wachache tu ndio watakaoponyoka katika vita na kurudi kutoka inchi ya Misri na kwenda katika inchi ya Yuda. Halafu Wayuda wote waliobaki kati ya wale waliokwenda kukaa Misri watatambua ni neno la nani lenye nguvu: langu au lao! Nitawaazibu hapahapa mupate kujua kwamba maneno ya hasara niliyosema juu yenu yatatimia. –Ni ujumbe wa Yawe.– Na hiki kitakuwa kitambulisho chake: Nitamutia Hofura mufalme wa Misri katika mikono ya waadui zake, katika mikono ya wale wanaotaka kumwua kama vile nilivyomutia Zedekia mufalme wa Yuda, katika mikono ya waadui zake ni kusema Nebukadneza, mufalme wa Babeli, ambaye alitaka kumwua. Ni Yawe anayesema hivyo. Haya ndiyo maneno nabii Yeremia aliyosema katika mwaka wa ine wa utawala wa Yoyakimu mwana wa Yosia, mufalme wa Yuda na Baruku mwana wa Neria akayaandika katika kitabu: Yawe, Mungu wa Israeli, anasema hivi juu yako wewe Baruku: Wewe ulisema: Ole wangu! Yawe ameongezea uchungu juu ya maumivu yangu. Nimechoka na kulalamika, wala siwezi kupumzika. Lakini Yawe ameniambia nikuambie: Yawe anasema hivi: Yale niliyojenga ninayabomoa, na yale niliyopanda ninayaongoa; nitafanya hivyo katika inchi yote. Wewe unajitakia wewe mwenyewe mambo makubwamakubwa? Usiyatafute! Achana nayo, maana ninaleta maangamizi juu ya wanadamu wote. Pato lako ni hili: nitayaokoa maisha yako kila nafasi utakapokwenda. –Ni ujumbe wa Yawe. Yawe akamutolea Yeremia ujumbe juu ya watu wa mataifa. Juu ya Misri na jeshi la Neko mufalme wa Misri, lililokuwa huko Karkemisi karibu na muto Furati ambalo Nebukadneza mufalme wa Babeli alilishambulia katika mwaka wa ine wa utawala wa Yoyakimu mwana wa Yosia, mufalme wa Yuda: Mutayarishe ngao ndogo na kubwa musonge mbele kwa kupigana vita. Mutandike farasi na kupanda juu yao. Mushike nafasi zenu, na muvae kofia za chuma. Munoe mikuki yenu, muvae nguo zenu za chuma. Lakini mbona ninawaona wametishwa? Wamerudi nyuma. Mashujaa wao wamepigwa, wamekimbia mbio, bila hata kuangalia nyuma. Kuna kitisho kila upande. –Ni ujumbe wa Yawe.– Wanaokuwa wepesi hawawezi kutoroka, mashujaa hawawezi kukwepa; huko kaskazini kwenye muto Furati wamejikwaa na kuanguka. Nani huyo anayekuwa kama muto Nili uliofurika, kama mito inayovumisha mawimbi? Misri ni kama muto Nili uliofurika, kama mito inayovumisha mawimbi. Ilisema: Nitajaa, nitaifunika inchi, nitaiharibu miji na wakaaji wake. Musonge mbele, enyi farasi; mushambulie, enyi magari ya vita. Mashujaa wasonge mbele: watu wa Etiopia na Puti wanaoshika ngao, watu wa Ludi, wafundi wa kutumia pinde. Lakini siku hiyo ni siku ya Bwana wetu Yawe wa majeshi. Ni siku ya kulipiza kisasi, siku ya kuwaazibu waadui zake. Upanga utawamaliza hao na kutosheka, utaikunywa damu yao na kushiba. Maana Bwana wetu Yawe wa majeshi yuko na sadaka huko kaskazini karibu na muto Furati. Mupande Gileadi, enyi watu wa Misri, kwa kutafuta dawa. Mumetumia dawa nyingi bure; hakuna kitakachowaponyesha ninyi. Mataifa yamesikia jinsi mulivyopata haya, kilio chenu kimeenea katika dunia yote; mashujaa wamegongana wenyewe kwa wenyewe, wote pamoja wameanguka. Hili ndilo neno ambalo Yawe alimwambia Yeremia wakati Nebukadneza mufalme wa Babeli alipofika kuishambulia inchi ya Misri: Tangaza katika inchi ya Misri, uijulishe huko Migidoli, uijulishe huko Nofi na Tapanesi. Uwaambie: Mukae tayari kabisa maana upanga utawaangamiza kila nafasi. Kwa nini shujaa wako amekimbia? Mbona ngombe dume wako hakuweza kuvumilia? Kwa sababu mimi Yawe nilimwangusha chini! Wengi walijikwaa, wakaanguka, kisha wakaambiana wao kwa wao: Musimame, tuwaendee watu wetu, turudi katika inchi yetu, tuukimbie upanga wa adui. Naye Mufalme wa Misri, mumupange jina hili: Mwenye domo ya bure! Kama vile ninavyoishi, –ni ujumbe wa mufalme, jina lake Yawe wa majeshi– kweli adui anakuja kuwashambulia: ni hakika kama vile Tabori unavyokuwa mulima, kama vile mulima Karmeli unavyoonekana kutoka katika bahari. Enyi wakaaji wa Misri, mujitayarishe na mizigo kwenda katika uhamisho! Maana muji wa Nofi utaharibiwa kabisa, utakuwa mabomoko yasiyokaliwa na watu. Misri ni kama mwana-ngombe muzuri, lakini uharibifu kutoka kaskazini umekuja juu yake. Hata waaskari wake wa mushahara ni kama wana-ngombe wanono; nao tena wamegeuka, wakakimbia pamoja, wala hawakuweza kuvumilia, kwa maana siku yao ya kuangamizwa imefika, wakati wao wa kuazibiwa umetimia. Misri anatoroka bila fujo kama nyoka anayekimbia; maana waadui zake wanamufikia kwa nguvu, wanamufikia kwa mashoka kama wakata miti. Watakata kabisa pori lake, ingawa halipenyeki. –Ni ujumbe wa Yawe– maana wao ni wengi kuliko nzige wasiohesabika. Watu wa Misri watapata haya, watatiwa katika mikono ya watu kutoka kaskazini. Yawe wa majeshi, Mungu wa Israeli, alisema: Mimi nitamwazibu Amoni mungu wa muji wa Tebesi, nitaiazibu Misri na miungu yake na wafalme wake, nitamwazibu Mufalme wa Misri na wote wanaomutegemea. Nitawatia katika mikono ya wale wanaotaka kuyaangamiza maisha yao, ni kusema Nebukadneza mufalme wa Babeli na wakubwa wake. Kisha, inchi ya Misri itakaliwa na watu kama ilivyokuwa hapo zamani. –Ni ujumbe wa Yawe. Lakini wewe usiogope, ee Yakobo mutumishi wangu, usifazaike, ee Israeli, maana nitakuokoa kutoka mbali, nitakuja kuwaokoa wazao wako kutoka inchi walimohamishiwa. Yakobo utarudi na kutulia na kustarehe, wala hakuna yeyote atakayekutia hofu. Usiogope, ee Yakobo mutumishi wangu, kwa maana mimi niko pamoja nawe. –Ni ujumbe wa Yawe.– Nitayaangamiza kabisa mataifa yote ambayo nimekutawanya kati yao, lakini wewe sitakuangamiza. Nitakuazibu kadiri unavyostahili, sitakuacha bila kukuazibu. Hili ni neno Yawe alilomwambia nabii Yeremia juu ya Wafilistini, mbele mufalme wa Misri hajaushambulia muji wa Gaza: Yawe anasema hivi: Maji yanapanda kutoka kaskazini, nayo yatakuwa muto uliofurika; yataifunika inchi nzima na vyote vinavyokuwa ndani yake, muji na wakaaji na wanaoishi humo. Watu watalia, wakaaji wote wa inchi wataomboleza. Watasikia shindo la kwato za farasi, kelele za magari ya vita, na vishindo vya magurudumu yao. Wababa watawasahau watoto wao, mikono yao itakuwa imeregea sana. Hiyo ni siku ya kuwaangamiza Wafilistini wote, kukomesha musaada uliobakia kutoka Tiro na Sidona. Maana Yawe anawaangamiza Wafilistini, watu waliobaki wa kisanga cha Kafutori. Watu wa Gaza wamenyoa kichwa kwa kuomboleza; muji wa Askeloni umeangamia. Enyi watu muliobaki katika bonde mutajikatakata kwa huzuni mpaka wakati gani? Ee upanga wa Yawe! Utatwaa muda gani ndipo utulie? Ingia katika mufuko wako, upate kutulia na kunyamaza! Lakini utaweza kutulia namna gani, ikiwa ni Yawe ameupa kazi? Ameuamuru ushambulie muji wa Askeloni na watu wanaoishi kandokando ya bahari. Juu ya inchi ya Moabu, Yawe wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi: Ole kwa watu wa Nebo, maana muji wao umeharibiwa! Kiriataimu umepatishwa haya, umetekwa, ukuta wake umebomolewa; utukufu wa inchi ya Moabu umetoweka. Mupango ulifanywa huko Hesiboni juu yake: Basi! Tuwaangamize wasikuwe tena taifa! Nawe muji wa Madimeni utanyamazishwa, upanga utakufuatilia. Sikiliza! Kilio kutoka Horonaimu: Maangamizi na uharibifu mukubwa! Moabu imekwisha kuangamizwa, kilio chake kinasikilika mpaka Zoari. Wale wanaopanda kwenda Luhiti wanalia kwa sauti. Wanapoteremuka kwenda Horonaimu, wanasikia kilio cha uharibifu. Mukimbie! Mujiokoe wenyewe! Mukimbie kama punda wa pori katika jangwa! Moabu, ulitumainia matendo yako na hazina zako, lakini sasa wewe vilevile utatekwa; mungu wako Kemosi atapelekwa katika uhamisho pamoja na makuhani na watumishi wake. Mwangamizaji atapita katika kila muji, hakuna muji utakaomwepuka; mabonde yataangamia, nafasi zenye kunyooka zitaharibiwa, kama vile Yawe alivyosema. Muchimbie Moabu kaburi, maana kuangamia kwake ni hakika; miji yake itakuwa tupu, bila mukaaji hata mumoja. Alaaniwe mutu anayefanya kazi ya Yawe kwa uregevu; alaaniwe anayezuia upanga wake usimwange damu! Moabu amestarehe tangu ujana wake, ametulia kama divai katika mutungi. Hajamimiliwa toka chombo kimoja katika chombo kingine, hajapata kupelekwa katika uhamisho. Kwa hiyo angali na onjo yake, harufu yake nzuri haijabadilika hata kidogo. Kwa hiyo, siku zinakuja ambapo nitamupelekea wamimiaji ambao wataimimia divai yake. –Ni ujumbe wa Yawe.– Wataimwanga yote kutoka vyombo vyake na kuvivunja vipandevipande. Halafu Wamoabu watapata haya kwa ajili ya mungu wao Kemosi, kama vile watu wa Israeli walivyopata haya kwa ajili ya kutegemea Beteli. Namna gani munaweza kusema: Sisi ni mashujaa, na watu wenye nguvu nyingi za vita? Mwangamizaji wa Moabu na miji yake anashambulia, vijana wake wazuri wamechinjwa. –Ni ujumbe wa Mufalme, jina lake Yawe wa majeshi.– Uharibifu wa Moabu umekaribia, maangamizi yake yanakuja haraka. Muomboleze juu ya Moabu, enyi wajirani zake wote, na wote munaomujua vizuri museme: Namna gani nguvu kama hii ilivunjwa, uwezo ule wenye utukufu? Enyi wenyeji wa Diboni: mushuke kutoka pahali penu pa utukufu, muikae juu ya udongo usiokuwa na maji. Maana mwangamizaji wa Moabu, amefika kuwashambulia; amekwisha haribu kuta zenu. Enyi wakaaji wa Aroeri, musimame kandokando ya njia mupeleleze! Mumwulize yule anayekimbia na anayetoroka: Kumetokea nini? Moabu imepatishwa haya maana imevunjika. Muomboleze na kuililia. Mutangaze kandokando ya muto Arnoni, kwamba Moabu imeharibika kabisa. Hukumu imeifikia miji ya nafasi ya uwanja: Holoni, Yahasa, Mefati, Diboni, Nebo, Beti-Diblataimu, Kiriataimu, Beti-Gamuli, Beti-Meoni, Kerioti na Bosira. Kweli, hukumu imeifikia miji yote ya Moabu ya mbali na ya karibu. Nguvu za Moabu zimevunjika na uwezo wake umevunjika. –Ni ujumbe wa Yawe.– Mumuleweshe Moabu kwa sababu alijitukuza juu yangu mimi Yawe. Moabu atagaagaa katika matapiko yake na watu watamuchekelea. Ee Moabu, si ulimuchekelea Israeli! Ulimuhesabu kama mwenzake na wanyanganyi hata ukakuwa unatikisa kichwa chako kila mara uliposema juu yake. Enyi wenyeji wa Moabu, mutoke katika miji, muende kukaa chini ya mawe! Muige jinsi njiwa anavyojenga chicha chini ya jiwe. Tumesikia juu ya kiburi cha Moabu; Moabu ana majivuno sana. Tumesikia juu ya kujiona, kiburi na majivuno yake; tumesikia jinsi anavyojisifu ndani ya moyo. Ninajua kiburi chake. –Ni ujumbe wa Yawe.– Majivuno yake ni ya bure, na matendo yake si kitu. Kwa hiyo ninaomboleza juu ya Moabu, ninalia kwa ajili ya Wamoabu wote, ninaomboleza juu ya watu wa Kiri-Heresi. Ninakulilia wewe muzabibu wa Sibuma kuliko hata watu wa Yazeri. Matawi yako yametanda mpaka ngambo ya bahari ya Chumvi, yakafika hata mpaka Yazeri. Lakini mwangamizaji ameyarukia matunda yako ya wakati wa jua na mizabibu yako. Furaha na shangwe zimeondolewa kutoka inchi ya Moabu yenye mboleo. Nimeikomesha divai kutoka katika vikamulio. Hakuna mutu anayekamua mizabibu kwa shangwe; kelele zinazosikilika si za shangwe. Kilio cha watu wa Hesiboni kinasikilika huko Eleale mpaka Yasa; kinaenea kutoka Soari mpaka Horonaimu na kufika hata Eglati-Selisia. Hata maji ya kijito Nimurimu yamekauka. Nami nitamuteketeza kila mutu katika Moabu ambaye anatambikia juu ya vilima na kumufukizia mungu wake ubani. –Ni ujumbe wa Yawe. Kwa hiyo, moyo wangu unaomboleza juu ya watu wa Moabu na watu wa Kiri-Heresi, kama vile filimbi; maana hata mali yote waliyojipatia imeangamia. Kila mutu amenyoa kichwa na ndevu zake. Wote wamejikatakata kwenye mikono na kwenye viuno wamevaa gunia. Juu ya nyumba za Moabu na katika viwanja vyao hakuna kinachosikilika lakini maombolezo tu. Mimi nimemuvunja Moabu kama chombo kisichotakiwa na mutu. –Ni ujumbe wa Yawe. Angalia jinsi alivyovunjika! Angalia jinsi wanavyoomboleza! Ni ajabu jinsi Moabu alivyorudi nyuma juu ya haya! Moabu amekuwa kitu cha kuchekesha na kitisho kwa jirani zake wote. Yawe anasema hivi: Taifa litaruka mbio juu ya Moabu, kama tai aliyekunjua mabawa yake. Miji yake itatekwa, kuta zake vilevile. Siku hiyo mioyo ya waaskari wa Moabu itakuwa kama vile moyo wa mwanamuke anayezaa. Wamoabu wataangamizwa, hata hawatakuwa tena taifa, kwa sababu walijitukuza mbele ya Yawe. Kitisho, mashimo na mutego, vinawangojea enyi watu wa Moabu. –Ni ujumbe wa Yawe. Atakayetoroka kitisho atatumbukia ndani ya shimo; atakayetoka ndani ya shimo atanaswa katika mutego. Kwa maana nitaleta mambo hayo juu ya Moabu, katika mwaka wao wa azabu. –Ni ujumbe wa Yawe. Wakimbizi wanaochoka wanasimama chini ya kivuli cha Hesiboni. Moto umewaka huko katika muji; ulimi wa moto toka nyumba ya kifalme ya Sihoni; umeteketeza mipaka ya Moabu, umeunguza milima ya hao wanaopiga kelele. Ole kwenu watu wa Moabu! Watu wa Kemosi sasa mumeangamizwa, wana wenu wamekamatwa mateka, wabinti zenu wamepelekwa katika utumwa. Lakini katika siku zinazokuja nitawarudisha tena Moabu katika hali yao. –Ni ujumbe wa Yawe. Hii ndiyo hukumu juu ya Moabu. Juu ya Waamoni, Yawe anasema hivi: Israeli hana watoto? Hana warizi? Mbona basi mungu Milkomu ametwaa Gadi na watu wake wanafanya makao yao katika miji yake? Kwa hiyo, siku zinakuja ambapo nitavumisha sauti ya vita juu ya Raba muji wa Waamoni. –Ni ujumbe wa Yawe.– Raba utakuwa lundo la uharibifu, vijiji vyake vitateketezwa kwa moto. Halafu Israeli atatwaa tena urizi wake. Ni Yawe anayesema hivyo. Muomboleze, enyi watu wa Hesiboni, maana muji Ai umeharibika! Mulie, enyi wabinti wa Raba! Muvae magunia, muomboleze na kukimbia huko na huko ndani ya ukuta wenu! Maana mungu Milkomu atapelekwa katika uhamisho, pamoja na makuhani wake na watumishi wake. Mbona munajivunia mabonde yenu, enyi musiokuwa waaminifu, ninyi watu muliotegemea mali zenu, mukisema: Nani atasubutu kupigana nasi? Basi, mimi nitawaletea vitisho. –Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe wa majeshi.– Hivi vitisho vitatoka kwa wajirani zenu wote, nanyi mutafukuzwa inje, kila mutu kwa njia yake, wala hakuna mutu atakayekusanya wakimbizi. Lakini kisha nitawarudisha tena Waamoni katika hali yao. –Ni ujumbe wa Yawe. Juu ya Edomu, Yawe wa majeshi anasema hivi: Hakuna tena hekima katika muji wa Temani? Wenye hekima wao hawana shauri tena? Hekima imetoweka kabisa? Mukimbie, enyi wakaaji wa Dedani, mugeuke na kujificha ndani ya mapango! Maana nitawaletea maangamizi, enyi wazao wa Esau; wakati wa kuwaazibu umefika. Wachuma zabibu watakapokuja kwenu, hawataacha hata zabibu moja. Usiku ule wizi watakapofika, wataharibu kila kitu mpaka watosheke. Lakini nimemunyanganya Esau kila kitu, nimeyafunua maficho yake, wala hawezi kujificha tena. Watoto, wandugu na jirani zake wameangamizwa; hakuna hata mumoja aliyebaki. Muniachie watoto wenu wayatima nami nitawatunza; muwaache wajane wenu wanitegemee. Yawe anasema hivi: Ikiwa wale ambao hawakustahili kunywa kikombe cha azabu ni lazima wakikunywe, basi, wewe utaachwa bila kuazibiwa? Hapana! Hautakosa kuazibiwa; ni lazima ukunywe hicho kikombe! Maana nimeapa kwa nafsi yangu kwamba muji wa Bosira utakuwa kitisho na mushangao, utakuwa uharibifu na kutumiwa kama mufano wa laana; vijiji vyote vitakuwa mabomoko siku zote. –Ni ujumbe wa Yawe. Nimepata habari kutoka kwa Yawe, na mujumbe ametumwa ayatangazie mataifa: Mujikusanye pamoja juu ya Edomu; musimame muende kushambulia! Mimi Yawe nitakufanya wewe Edomu kuwa mudogo kuliko mataifa yote. Ulimwengu wote utakuzarau. Vitisho unavyotoa na kiburi chako vimekudanganya, ewe unayekaa katika mapango ya mawe, unayeishi juu ya kilele cha mulima! Ingawa unaweka makao yako juu kama ya tai, mimi nitakuporomosha kutoka huko unakokuwa. –Ni ujumbe wa Yawe. Inchi ya Edomu itakuwa kitisho na kila mutu atakayepita karibu yake atashangaa, na kuizomea kwa sababu ya hasara itakayoipata. Kama vile Sodoma na Gomora na miji jirani yake ilivyoangamizwa, hakutakuwa mutu yeyote atakayeishi Edomu wala kufanya mashauri humo. –Ni Yawe anayesema.– Kama vile simba anavyochomoka kutoka ndani ya vichaka vya muto Yordani na kuingia kwenye mbuga, ndivyo nitakavyowafukuza kwa rafla Waedomu toka katika inchi yao. Nami nitamuweka huko mutawala yeyote nitakayemuchagua. Maana, ni nani anayeweza kulinganishwa nami? Nani anayeweza kunishitaki? Ni muchungaji gani anayeweza kunipinga? Kwa hiyo, musikilize mupango ambao mimi Yawe nimepanga juu ya Edomu pamoja na mambo niliyokusudia kuwafanyia wakaaji wa Temani: Hakika, watoto wao wadogo watakokotwa na kukamatwa; kweli kutakuwa mushangao mukubwa katika makao yao! Kwa kishindo cha kuanguka kwao, dunia itatetemeka, na kilio chao kitasikilika mpaka kwenye bahari Nyekundu. Adui atapanda juu na kuruka kama tai na kutandaza mabawa yake juu ya Bosira. Siku hiyo moyo wa mashujaa wa Edomu utakuwa kama vile moyo wa mwanamuke anayezaa. Hii ni juu ya Damasiki: Miji ya Hamati na Arpadi, imejaa wasiwasi kwa kufikiwa na habari mbaya; mioyo ya watu wake inayeyuka kwa hofu, imefazaika kama bahari isiyoweza kutulia. Watu wa Damasiki wamevunjika moyo; wamegeuka kusudi wapate kukimbia; hofu kubwa imewashika, uchungu na huzuni vimewapata, kama mwanamuke anayezaa. Namna gani muji wenye sifa umeachwa, muji uliokuwa umejaa furaha! Basi vijana wake wataanguka katika viwanja vyake, waaskari wake wote wataangamizwa siku hiyo. –Ni ujumbe wa Yawe wa majeshi. Nitawasha moto katika kuta za Damasiki, nao utateketeza nyumba nzuri za mufalme Beni-Hadadi. Juu ya Kedari na falme za Hazori ambazo Nebukadneza mufalme wa Babeli alizishambulia na kuzishinda, Yawe anasema hivi: Simama uende kulishambulia kabila la Kedari! Uwaangamize watu wa mashariki! Hema zao na kondoo wao vitakamatwa, vilevile na mapazia yao na mali yao yote; watanyanganywa ngamia wao, na kilio kitasikilika: Kitisho kila upande! Mukimbie, muende mbali, mukae ndani ya mashimo. Enyi wakaaji wa Hazori, mukimbie, mutangetange na kujificha mbali! –Ni ujumbe wa Yawe.– Maana Nebukadneza mufalme wa Babeli, amefanya mupango juu yenu, amekusudia kuja kuwashambulia. Simama uende kulishambulia taifa linalostarehe, taifa linaloishi kwa usalama. –Ni ujumbe wa Yawe.– Taifa hilo halina milango wala vifungio vya chuma; ni taifa ambalo liko peke yake. Ngamia wao watatekwa, makundi yao ya nyama yatanyanganywa. Nitawasambaza kila upande, watu wale wanaonyoa nywele zote za pembenipembeni ya kichwa. Nitawaletea hasara kutoka kila upande. –Ni ujumbe wa Yawe. Muji wa Hazori utakuwa makao ya mbweha, utakuwa jangwa siku zote; hakuna mutu atakayekaa humo, wala atakayeishi humo. Yawe akamutolea nabii Yeremia ujumbe huu juu ya Elamu, kwa mwanzo wa utawala wa Zedekia, mufalme wa Yuda. Yawe wa majeshi anasema hivi: Nitavunja upinde wa watu wa Elamu unaokuwa musingi wa nguvu zao. Nitaleta upepo kutoka pande zote za mbingu; nitawatawanya kila pahali, wala hakutakuwa taifa lolote ambalo halitakuwa na wakimbizi wa Elamu. Nitawafazaisha watu wa Elamu mbele ya waadui zao na mbele ya wale wanaotaka kuyaangamiza maisha yao. Nitawaletea hasara na hasira yangu kali. –Ni ujumbe wa Yawe.– Nitawashambulia kwa upanga mpaka niwaangamize kabisa. Nitaweka kiti changu cha kifalme huko Elamu na kumwangamiza mufalme wao pamoja na wakubwa wao. –Ni ujumbe wa Yawe! Lakini katika siku za mwisho, nitaurudishia muji wa Elamu hali yake. –Ni ujumbe wa Yawe! Yawe akatoa ujumbe huu kwa njia ya nabii Yeremia juu ya inchi ya Babeli, ile inchi ya Wakaldea: Mutangaze kati ya mataifa, munyanyue bendera na kutangaza, musifiche jambo lolote. Museme: Babeli umetekwa, mungu Beli amepatishwa haya. Merodaki amefazaishwa; sanamu zake zimefezeheshwa, miungu yake imefazaishwa. Kwa maana, taifa kutoka kaskazini limefika kuushambulia; litaifanya inchi yake kuwa uharibifu. Hakuna atakeyeishi humo; watu na nyama watakimbia mbali. Siku hizo na wakati huo, watu wa Israeli na watu wa Yuda watakusanyika pamoja na kuja wakilia na kutafuta Yawe, Mungu wao. –Ni ujumbe wa Yawe. Watauliza njia ya kwenda Sayuni, na nyuso zao zikielekea huko, wakisema: Mukuje! Nao watajiunga na Yawe katika agano la milele ambalo halitasahauliwa hata kidogo. Watu wangu walikuwa kama kondoo waliopotea; wachungaji wao wamewapotosha, wakawageuza kuelekea kwenye milima; walitembea toka mulima mpaka kilima, wakasahau makao yao. Watu wote waliowakuta waliwaua, na waadui zao wamesema: Sisi hatuna kosa, maana hao wamemukosea Yawe anayekuwa makao yao ya kweli; Yawe ambaye ni tegemeo la babu zao! Mukimbie kutoka Babeli! Mutoke inje ya ile inchi ya Wakaldea, mukuwe kama mabeberu mbele ya kundi. Maana, mimi nitachochea mataifa makubwa kutoka inchi ya kaskazini washambulie inchi ya Babeli. Watajitayarisha kuishambulia inchi ya Babeli na kuiteka. Mishale yao ni kama shujaa hodari asiyerudi mikono mitupu. Inchi ya Wakaldea itanyanganywa, na hao watakaoinyanganya watashiba. –Ni ujumbe wa Yawe. Enyi wanyanganyi wa mali yangu, ijapokuwa munafurahi na kushangilia, munarukaruka kama mwana-ngombe anayepepeta ngano, na kulia kama farasi dume, lakini inchi yenu ya kuzaliwa itapatishwa haya; hiyo inchi mama yenu, itafezeheshwa. Babeli itakuwa ya mwisho kati ya mataifa, itakuwa mbuga yenye kukauka na jangwa. Kwa sababu ya kasirani yangu Yawe, Babeli haitakaliwa kabisa na watu, lakini itakuwa jangwa kabisa; kila mutu atakayepita karibu nayo atashangaa, ataizomea kwa sababu ya mapigo yake. Enyi wafundi wote wapiga mishale, mujipange kwa kuzunguka muji wa Babeli kwa vita; mupige mishale, musiache mushale hata mumoja, maana umenikosea mimi Yawe. Mupigie kelele za vita pande zote; sasa Babeli umejitoa ukamatwe. Vikingio vyote vimeanguka, kuta zake zimebomolewa. Ni malipizi ya Yawe. Basi muulipize kisasi. Muutendee kama vile ulivyotendea wengine. Muzuie watu wasipande mbegu Babeli, wala wasivune wakati wa mavuno. Kutokana na upanga wa uharibifu, kila mumoja atawarudilia watu wake, kila mumoja atakimbilia katika inchi yake. Israeli ni kama kondoo wanaowindwa na kufukuzwa na simba. Kwanza waliangamizwa na mufalme wa Asuria, na sasa Nebukadneza mufalme wa Babeli, amevunjavunja mifupa yake. Kwa hiyo Yawe wa majeshi, Mungu wa Israeli anasema hivi: Nitamwazibu mufalme wa Babeli na inchi yake, kama nilivyomwazibu mufalme wa Asuria. Nitawarudisha Waisraeli katika inchi yao, nao watakula mavuno yatakayolimwa juu ya mulima Karmeli na Basani na watatosheka kwa chakula kutoka milima ya Efuraimu na Gileadi. Siku hizo na wakati huo, uovu utatafutiwa katika inchi ya Israeli, lakini hautapatikana; zambi itatafutiwa katika inchi ya Yuda, lakini haitapatikana; maana mimi nitawasamehe wale ambao nimewaponyesha. –Ni ujumbe wa Yawe. Mupande, muiendee inchi ya Merataimu, muende kuishambulia; muwashambulie wakaaji wa Pekodi na kuwaangamiza kabisa watu wake. –Ni ujumbe wa Yawe.– Mufanye kila kitu nilichowaamuru. Kelele za vita zinasikilika katika inchi, kuna uharibifu mukubwa. Jinsi gani huo muji uliokuwa nyundo iliyoponda dunia nzima unavyoangushwa chini na kuvunjika! Babeli umekuwa pori tupu kati ya mataifa! Ewe Babeli, nilikutegea mutego ukanaswa, wala haukujua kitu juu yake; ulipatikana, ukakamatwa, kwa sababu ulishindana nami Yawe. Nimefungua gala yangu ya silaha, nikatoa humo silaha za kasirani yangu, maana mimi Bwana wa wote, Yawe wa majeshi, nina kazi ya kufanya katika inchi ya Wakaldea. Mukuje kumushambulia kutoka kila upande; muzifungue gala zake za chakula; mumulundikie malundo ya ngano! Muiangamize kabisa inchi hii; musiache kitu chochote! Muwaue waaskari wake hodari; muache washukie kwenye machinjo. Ole kwao, maana siku yao imetimia, wakati wao wa kuazibiwa umefika! Sikiliza! Wakimbizi na wenye kutoroka kutoka inchi ya Babeli wanakuja kutangaza huko Sayuni jinsi Yawe, Mungu wetu, alivyolipiza kisasi kwa ajili ya hekalu lake. Muwaite wapiga mishale waishambulie Babeli. Mupeleke kila mutu anayejua kuvuta upinde. Muuzunguke muji kusikuwe mutu yeyote atakayetoroka. Muulipize kadiri ya matendo yake yote; muutendee kama ulivyowatendea wengine, maana kwa kiburi ulinizarau mimi Yawe, Mutakatifu wa Israeli. Kwa hiyo, vijana wake watauawa katika mabarabara yake, na makundi yake yote ya waaskari yataangamizwa siku hiyo. –Ni ujumbe wa Yawe. Mimi, ninapigana nawe, ewe mwenye kiburi. –Ni ujumbe wa Bwana wa wote, Yawe wa majeshi.– Maana siku yako ya azabu imefika, wakati nitakapokuazibu umetimia. Mwenye kiburi atajikwaa na kuanguka, wala hakutakuwa mutu wa kumwinua. Nitawasha moto katika miji yake, nao utateketeza kila kitu kandokando yake. Yawe wa majeshi anasema hivi: Watu wa Israeli wanagandamizwa pamoja na watu wa Yuda. Wale waliokamata mateka wamewabana sana na wanakataa kuwaachilia. Lakini mimi, Mukombozi wao ni mwenye nguvu. Yawe wa majeshi ndilo jina langu. Hakika nitatetea maneno yao kusudi nilete amani katika inchi yao, lakini taabu kwa wakaaji wa Babeli. Upanga ukuwe juu ya Wakaldea, juu ya wakaaji wa Babeli na wakubwa na wenye hekima wake! –Ni ujumbe wa Yawe.– Upanga ukuwe juu ya waaguzi, kusudi wakuwe wapumbafu! Upanga ukuwe juu ya mashujaa, kusudi waangamizwe! Upanga ukuwe juu ya farasi wake na magari yake, juu ya majeshi yake yote ya mushahara, kusudi wakuwe sawa na wanawake! Upanga ukuwe juu ya hazina zake zote kusudi zinyanganywe. Jua kali liyapige maji, kusudi yapate kukauka! Maana Babeli ni inchi inayojaa sanamu za miungu, watu ni wenda-wazimu kwa sababu ya miungu yao. Kwa hiyo nyama wa pori, imbwa wa pori pamoja na mbuni, watakaa Babeli. Hakutakaliwa hata kidogo na watu wa vizazi vyote vinavyokuja. Kama vile mimi Yawe nilivyoiangamiza miji ya Sodoma na Gomora na miji ya jirani, vilevile hakutakuwa mutu yeyote atakayeishi humo. Kweli, hakuna mutu yeyote atakeyekaa huko. –Ni ujumbe wa Yawe. Muangalie! Watu wanakuja toka inchi ya kaskazini; taifa kubwa na wafalme wengi linajitayarisha kutoka mbali kwa miisho ya dunia. Wameshika pinde zao na mikuki; ni watu wakali wasiokuwa na huruma. Vishindo vyao ni kama uvumi wa bahari, wamepanda juu ya farasi. Wamejipanga tayari kwa vita na wewe Babeli! Mufalme wa Babeli amesikia habari zao. Kwa hiyo, mikono yake ikaregea. Ameshikwa na huzuni na uchungu, kama mama anayezaa. Kama vile simba anavyotoka ndani ya vichaka vya muto Yordani na kuingia kwenye mbuga, ndivyo nitakavyowafukuza kwa rafla watu wake kutoka kwake. Nami nitamuweka huko mutawala yeyote nitakayemuchagua. Maana, ni nani anayeweza kulinganishwa nami? Nani anayeweza kunishitaki? Ni muchungaji gani anayeweza kunipinga? Kwa hiyo, musikilize mupango ambao Yawe amepanga juu ya Babeli pamoja na mambo aliyokusudia kuifanyia inchi ya Wakaldea: Hakika, watoto wao wadogo watakokotwa na kukamatwa; kweli kutakuwa mushangao mukubwa katika makao yao! Kwa kishindo cha kutekwa kwa Babeli, dunia itatetemeka, na kilio chake kitasikilika kati ya mataifa mengine. Yawe anasema hivi: Nitavumisha upepo wa kuangamiza juu ya Babeli na juu ya wakaaji wa Kaldea. Nitawapeleka wapepetaji katika inchi ya Babeli, nao watamupepeta; watamaliza kila kitu katika inchi yake watakapofika kuishambulia toka kila upande wakati wa maangamizi yake. Usiwape nafasi wapiga mushale wa Babeli; usiwaache wavute upinde, wala kuvaa nguo zao za vita. Usiwahurumie vijana wake; uangamize kabisa jeshi lake. Wataanguka na kuuawa katika inchi ya Wakaldea, wataumizwa katika barabara zake. Lakini Israeli na Yuda hawakuachiliwa na Mungu wao, Yawe wa majeshi, ingawa inchi yao imejaa makosa mbele ya Mutakatifu wa Israeli. Mukimbie kutoka Babeli, kila mutu apate kuyaokoa maisha yake! Musiangamizwe katika azabu yake, maana huu ndio wakati wa Mungu wa kulipiza kisasi, anaiazibu Babeli kama inavyostahili. Babeli ilikuwa kikombe cha zahabu katika mukono wa Yawe, ambacho kiliilewesha dunia nzima. Mataifa yalikunywa divai yake; kwa hiyo, yakapata wazimu. Kwa rafla Babeli imeanguka na kuvunjikavunjika; muomboleze kwa ajili yake! Mulete dawa kwa kutuliza maumivu yake; labda utaweza kupona. Tulijaribu kuuponyesha Babeli, lakini hauwezi kupona. Muuache, tujiendee, kila mumoja katika inchi yake. Hukumu yake ni kubwa sana inafika mpaka katika mawingu. Yawe amehakikisha kwamba hatuna kosa. Tuende Sayuni tutangaze matendo ya Yawe, Mungu wetu. Yawe amezichochea roho za wafalme wa Wamedi, kwa maana amekusudia kuiangamiza Babeli. Kweli, hicho ndicho kisasi cha Yawe; analipiza kisasi kwa ajili ya hekalu lake. Munoe mishale yenu! Mutwae ngao! Mupandishe bendera ya vita kwa kushambulia kuta za Babeli. Muimarishe walinzi, muweke walinzi, mutayarishe mashambulizi. Yawe amepanga na kutimiza mambo aliyosema juu ya wakaaji wa Babeli. Inchi hiyo imejaa mito na akiba tele, lakini mwisho wake umefika, uzi wa uzima wake umekatwa. Yawe wa majeshi ameapa kwa nafsi yake: Hakika nitakujaza na watu kama vile nzige, nao watapiga vigelegele vya ushindi juu yako. Yawe ndiye aliyeumba dunia kwa nguvu zake, aliyeuimarisha ulimwengu kwa hekima yake, na kwa akili yake akazitandaza mbingu. Anapotoa sauti yake maji yanajikusanya mbinguni, anafanya ukungu upande kutoka mipaka ya dunia. Anafanya umeme upige wakati wa mvua, anavumisha upepo kutoka gala zake. Kila mutu ni mupumbafu bila maarifa, kila mufua vyuma anapatishwa haya na miungu yake; maana sanamu zake ni udanganyifu mutupu, wala hazina pumzi ndani yake. Hazina maana, ni udanganyifu mutupu; wakati watakapoazibiwa, nazo zitaangamia. Mungu anayekuwa hazina ya Yakobo si kama hizo, maana yeye ndiye aliyeviumba vitu vyote, na Israeli ni kabila linalokuwa mali yake; Yawe wa majeshi, ndilo jina lake. Yawe anasema hivi: Wewe Babeli ni nyundo na silaha yangu ya vita; ninakutumia kwa kuyavunjavunja mataifa, ninakutumia kwa kuangamiza falme. Ninakutumia kwa kuponda farasi na waaskari wapanda-farasi, magari ya kukokotwa na watembezaji wake. Ninakutumia kwa kuwaponda wanaume na wanawake, wazee na vijana, vijana wanaume na wabinti. Ninakutumia kwa kuponda wachungaji na makundi yao, walimaji na nyama wao wanaotumia kwa kulima, wakubwa na maliwali. Nitaiazibu Babeli na wakaaji wote wa Kaldea mukiona kwa macho yenu wenyewe, kwa sababu ya uovu wote walioufanya katika Sayuni. –Ni ujumbe wa Yawe. Mimi ninapingana nawe, ewe mulima muharibifu, mulima unaoharibu dunia nzima! –Ni ujumbe wa Yawe.– Nitanyoosha mukono wangu juu yako kwa kukuazibu, nitakuangusha kutoka juu kwenye mawe makubwa na kukufanya kuwa mulima uliochomwa kwa moto. Kwako hakutapatikana jiwe la kujenga, hata jiwe kwa kujenga musingi! Utakuwa kama jangwa milele. –Ni ujumbe wa Yawe!– Pandisha bendera ya vita katika dunia, piga baragumu kati ya mataifa; uyatayarishe mataifa kwa kupigana naye; uziite falme kwa kuishambulia; falme za Ararati, Mini na Askenazi. Weka jemadari juu yake; ulete farasi kama makundi ya nzige. Mutayarishe mataifa kwa kupigana naye vita; muwatayarishe wafalme wa Medi, watawala na maliwali wao, mutayarishe inchi zote katika utawala wao. Inchi inatetemeka na kugaagaa kwa maumivu, maana nia ya Yawe juu ya Babeli ni imara: ataifanya inchi ya Babeli kuwa jangwa, ataifanya ikuwe bila watu. Waaskari wa Babeli wameshindwa kupigana, wamebaki katika makimbilio yao; nguvu zao zimewaishia, wamekuwa kama wanawake. Nyumba za Babeli zimechomwa kwa moto, milango yake ya chuma imevunjwa. Wakimbiaji wanakimbia wakitoleana ujumbe mumoja kwa mwingine kwa kumupasha mufalme wa Babeli habari kwamba muji wake umeshambuliwa kila upande. Vivuko vya muto vimetekwa, makimbilio yamechomwa kwa moto, waaskari wamepatwa na hofu. Yawe, Mungu wa Israeli, anasema hivi: Babeli ni kama uwanja wa kupepetea ngano wakati unapotayarishwa. Lakini bado kidogo tu, wakati wa mavuno utaufikia. Mufalme Nebukadneza wa Babeli aliuharibu na kuuponda Yerusalema aliuacha kama chungu kitupu; aliumeza kama vile nyoka mukubwa. Alijaza tumbo lake vitu vyake vizurivizuri, akautupilia mbali kama matapiko. Watu wa Sayuni watasema: Babeli ulipizwe mateso makali yaleyale tuliyotendewa sisi pamoja na jamaa zetu! Yerusalema itasema: Damu yangu ikuwe juu ya wakaaji wa Kaledea. Kwa hiyo Yawe anasema hivi: Nitawatetea juu ya maneno yenu, na kulipiza kisasi kwa ajili yenu. Nitaikausha bahari ya Babeli na kuvifanya visima vyake vikauke. Babeli itakuwa lundo la mabomoko, itakuwa makao ya mbweha, itakuwa machukizo na kitu cha kuzomewa; hakuna mutu atakayekaa ndani yake. Wababeli watanguruma pamoja kama simba; watalia kama wana-simba. Wakiwa na hamu kubwa nitawatayarishia karamu: nitawalewesha mpaka wapepesuke; nao watalala usingizi wa siku zote na hawataamuka tena. –Ni ujumbe wa Yawe.– Nitawashusha chini kama kondoo wa kuchinjwa, kama vile kondoo dume na beberu. Namna gani Babeli imetekwa; muji uliosifiwa katika dunia yote umekamatwa! Babeli umekuwa ukiwa kati ya mataifa! Bahari imefurika juu ya Babeli, Babeli imefunikwa na mawimbi yaliyochafuka. Miji yake imekuwa ukiwa, inchi yenye kukauka na jangwa, inchi isiyokaliwa na mutu yeyote, wala hakuna mwanadamu yeyote anayepita ndani yake. Nitamwazibu mungu Beli huko Babeli, nitamutapikisha kile alichomeza. Mataifa hayatamwendea tena kwa wingi. Ukuta wa Babeli umebomoka. Mutoke humo, enyi watu wangu! Kila mutu apate kuyaokoa maisha yake, kutoka hasira kali ya Yawe. Musiregee wala musikuwe na hofu, kwa sababu ya habari munazosikia katika inchi. Mwaka huu kuna habari hii, mwaka mwingine habari ingine; habari ya mateso makali katika inchi, mutawala mumoja anapigana na mutawala mwingine. Kwa hiyo, siku zinakuja ambapo nitaazibu sanamu za Babeli; inchi yake yote itapata haya, watu wake wote watauawa humohumo. –Ni ujumbe wa Yawe.– Kisha mbingu, dunia na vyote vinavyokuwa ndani yao vitaimba kwa furaha juu ya kuanguka kwa Babeli, wakati waangamizaji watakapofika kutoka upande wa kaskazini kuushambulia. –Ni ujumbe wa Yawe.– Babeli umesababisha vifo katika dunia yote; sasa muji wenyewe utaangamizwa kwa ajili ya mauaji ya Waisraeli. Ninyi mulioponyoka kifo, muondoke sasa, wala musisitesite! Ingawa muko katika inchi ya mbali, mumukumbuke Yawe, muukumbuke vilevile Yerusalema. Ninyi munasema: Tumepatishwa haya na kutukaniwa; haya imefunika nyuso zetu, kwa sababu wageni wameingia katika sehemu takatifu za nyumba ya Yawe. Kwa hiyo, siku zinakuja ambapo nitaiazibu miungu ya Babeli, na wenye kuumizwa watalalamika katika inchi yake yote. –Ni ujumbe wa Yawe.– Ingawa Babeli ungepanda mpaka mbinguni, na kuziimarisha kuta zake ndefu, waangamizaji watakuja kutoka kwangu kwa kuuharibu. –Ni ujumbe wa Yawe. Sikiliza! Kilio kinasikilika kutoka Babeli! Kishindo cha maangamizi makubwa kutoka inchi ya Wakaldea! Maana mimi Yawe ninaiangamiza Babeli, na kuikomesha kelele yake kubwa. Waadui wananguruma kama mawimbi ya maji mengi, sauti ya kishindo chao inaongezeka. Kweli, mwangamizaji anashambulia Babeli; waaskari wake wametekwa, pinde zao zimevunjwavunjwa. Mimi Yawe ni Mungu mwenye kuazibu, hakika mimi nitalipiza kisasi kamili. Nitawalewesha wakubwa na wenye hekima wake, watawala wake, maliwali na waaskari wake; watalala usingizi wa milele wala hawataweza tena kuamuka. –Ni ujumbe wa mufalme, jina lake Yawe wa majeshi! Yawe wa majeshi anasema hivi: Ukuta mukubwa wa Babeli utabomolewa mpaka chini, na milango yake mirefu itateketezwa kwa moto. Watu wanafanya juhudi za bure, mataifa yanajichokesha, maana mwisho wao ni katika moto! Katika mwaka wa ine wa utawala wake, mufalme Zedekia alikwenda Babeli pamoja na mukubwa wa wasimamizi wa nyumba yake anayeitwa Seraya mwana wa Neria na mujukuu wa Maseya. Wakati huo mimi Yeremia nilimutolea Seraya ujumbe. Nilikuwa nimeandika katika kitabu hasara yote niliyotangaza juu ya Babeli na vilevile maneno mengine juu ya Babeli. Nilimwambia Seraya: Utakapofika Babeli ni lazima uwasomee wote maneno haya. Kisha umalizie na maneno haya: Ee Yawe, wewe umesema kwamba utaharibu nafasi hii hata kusikaliwe na kiumbe chochote, mwanadamu au nyama, na kwamba inchi hii itakuwa jangwa milele. Utakapomaliza kusoma kitabu hiki, ufunge jiwe juu yake, kisha ukitumbukize katikati ya muto Furati, ukisema: Hivi ndivyo Babeli utakavyozama, wala hautainuka tena, kwa sababu ya hasara ambayo Yawe anauletea. Huu ndio mwisho wa maneno ya Yeremia. Zedekia alikuwa na umri wa miaka makumi mbili na mumoja alipoanza kutawala. Alitawala kwa muda wa miaka kumi na mumoja akiwa kule Yerusalema. Mama yake aliitwa Hamutali binti wa Yeremia, mukaaji wa muji wa Libuna. Alitenda maovu mbele ya Yawe akifuata yote Yoyakimu aliyofanya. Yawe aliwakasirikia sana watu wa Yerusalema na Yuda hata akawafukuza mbali naye. Zedekia alimwasi mufalme wa Babeli. Ikakuwa katika siku ya kumi ya mwezi wa kumi, mwaka wa kenda wa utawala wa Zedekia, Nebukadneza mufalme wa Babeli, alifika na waaskari wake wote kuushambulia Yerusalema, wakauzunguka kila upande. Muji uliendelea kuzungukwa mpaka mwaka wa kumi na mumoja wa utawala wa Zedekia. Katika siku ya kenda ya mwezi wa ine, njaa ilikuwa kali sana katika muji hata hakukukuwa chakula chochote kwa ajili ya wakaaji wake. Basi, sehemu ya ukuta wa muji ilibomolewa na waaskari walikimbia. Wakatoka inje ya muji wakati wa usiku wakipitia njia ya mulango katikati ya kuta mbili, kwenye bustani ya mufalme, ingawa Wakaldea walikuwa wameuzunguka muji wote. Wakakimbia kuelekea bonde la muto Yordani. Lakini kundi la Wakaldea lilimufuatilia mufalme na kumukamata katika bonde la Yeriko, waaskari wake wote wakatawanyika na kumwacha. Basi Wakaldea walimukamata mufalme, wakamupeleka kwa mufalme wa Babeli kule Ribla, katika inchi ya Hamati, naye akamuhukumu. Kulekule Ribla, mufalme wa Babeli aliwaua wana wa Zedekia mbele ya baba yao. Aliwaua vilevile wakubwa wote wa inchi ya Yuda. Kisha aliyaongoa macho ya Zedekia na kumufunga minyororo, akamupeleka Zedekia Babeli na kumutia katika kifungo mpaka siku alipokufa. Katika siku ya kumi ya mwezi wa tano, mwaka wa kumi na kenda wa utawala wa Nebukadneza, mufalme wa Babeli, Nebuzaradani mukubwa wa waaskari wa mufalme ambaye alimutumikia mufalme wa Babeli, aliingia Yerusalema. Aliteketeza kwa moto nyumba ya Yawe, nyumba ya kifalme na nyumba zote za Yerusalema; kila nyumba kubwa ilichomwa kwa moto. Waaskari wote wa Wakaldea waliokuwa pamoja na mukubwa wa waaskari, walizibomoa kuta zote zilizouzunguka Yerusalema. Nebuzaradani mukubwa wa waaskari wa mufalme, aliwapeleka katika uhamisho watu waliokuwa wamebakia katika muji na wale waliojitoa wenyewe kwa mufalme wa Babeli pamoja na wafundi. Lakini Nebuzaradani mukubwa wa waaskari walinzi wa mufalme, aliwaacha watu wamoja waliokuwa wamasikini kabisa katika inchi, wakuwe watunza mizabibu na walimaji. Wakaldea walivunja vipandevipande nguzo za shaba nyeusi ambazo zilikuwa katika nyumba ya Yawe pamoja na misingi ya birika kubwa la shaba nyeusi lililokuwa katika nyumba ya Yawe, wakapeleka shaba nyeusi yote mpaka Babeli. Vilevile, walipeleka vyungu, majembe, makasi, makarai, vijiko vikubwa na vyombo vyote vya shaba nyeusi vilivyotumiwa katika kazi ya hekalu. Yule mukubwa wa waaskari walinzi wa mufalme alipeleka vibakuli, vyetezo, mabeseni, vyungu, vinara vya taa, vijiko vikubwa na mabakuli ya sadaka za vinywaji, vyombo hivyo vikiwa vya zahabu au vya feza. Juu ya vitu Solomono alivyotengeneza: nguzo mbili, birika kubwa moja na sanamu za ngombe dume kumi na mbili za shaba nyeusi ambazo zilikuwa chini ya hilo birika kubwa pamoja na misingi, shaba nyeusi ya vitu hivi vyote ilikuwa na uzito mwingi sana. Kila moja ya nguzo hizo mbili ilikuwa na urefu wa metre nane, muzunguko wake metre tano na sentimetre makumi tatu, na unene wa sentimetre saba na nusu, zote zilikuwa wazi ndani. Juu ya kila nguzo kulikuwa kichwa cha shaba nyeusi; urefu wa kila kichwa ulikuwa metre mbili na sentimetre makumi mbili. Kila kichwa kilizungushiwa mapambo ya makomamanga, yote ya shaba nyeusi. Kulikuwa makomamanga makumi kenda na sita kwenye ubavu wa nguzo hizo; jumla ya makomamanga yote ilikuwa mia moja na mapambo kandokando yake. Kisha Nebuzaradani mukubwa wa waaskari walinzi wa mufalme, alimukamata Seraya Kuhani Mukubwa, na Zefania kuhani wa pili, pamoja na walinda mulango watatu; na kutoka katika muji alimukamata mukubwa mumoja ambaye alikuwa akiongoza waaskari katika vita, pamoja na watu saba washauri wa mufalme ambao aliwakuta katika muji. Alimukamata vilevile katibu wa jemadari mukubwa wa waaskari ambaye alishugulika na kazi ya kuandika waaskari wapya, pamoja na watu wakubwa makumi sita ambao aliwakuta katika muji Yerusalema. Nebuzaradani mukubwa wa waaskari walinzi wa mufalme, aliwakamata watu hao na kuwapeleka kwa mufalme wa Babeli kule Ribla. Mufalme Nebukadneza wa Babeli aliwapiga na kuwaua watu hao kule Ribla katika inchi ya Hamati. Basi, hivi ndivyo watu wa Yuda walikwenda katika uhamisho inje ya inchi yao. Hii ndiyo hesabu ya watu ambao Nebukadneza aliowapeleka katika uhamisho kwa mwaka wa saba wa utawala wake: Wayuda elfu tatu na makumi mbili na watatu. Mwaka wa kumi na nane na utawala wake, alipeleka kutoka Yerusalema watu mia nane makumi tatu na wawili. Mwaka wa makumi mbili na tatu wa utawala wa Nebukadneza, Nebuzaradani mukubwa wa waaskari walinzi wa mufalme, aliwapeleka Wayuda mia saba na makumi ine na watano. Jumla ya watu wote ilikuwa watu elfu ine mia sita. Katika mwaka wa makumi tatu na saba tangu Yoyakinu mufalme wa Yuda alipopelekwa katika uhamisho, siku ya makumi mbili na tano ya mwezi wa kumi na mbili, Ewili-Merodaki akakuwa mufalme wa Babeli. Mwaka uleule alipofanywa mufalme, alimusamehe Yoyakinu mufalme wa Yuda, akamwondoa katika kifungo. Aliongea naye vizuri na kumupatia nafasi ya heshima kuliko wafalme wengine waliokuwa pamoja naye katika uhamisho kule Babeli. Basi, Yoyakinu alibadilisha nguo zake za wafungwa, akakuwa anapata chakula chake siku zote kwenye meza ya mufalme. Siku zote alipewa posho na mufalme wa Babeli kulingana na mahitaji yake ya kila siku, mpaka alipokufa. Namna gani muji uliokuwa umejaa watu, sasa unakaa peke yake! Ulikuwa na utukufu kati ya mataifa, sasa umekuwa kama mama mujane. Ulikuwa kama binti wa mufalme kati ya miji, sasa umekuwa mutumwa. Unalia usiku kucha; machozi yanatiririka juu ya mashavu yake. Hakuna hata mumoja kati ya wapenzi wake kwa kuufariji. Rafiki zake wote wameudanganya; wamekuwa waadui zake. Watu wa Yuda wamekwenda katika uhamisho, wakijaa mateso na kuwa katika utumwa mukali. Wanakaa kati ya watu wa mataifa, wala hawapati nafasi ya kupumzikia. Waliowafuatilia wamewakamata wakiwa katika taabu. Barabara za Sayuni zinaomboleza, maana hakuna anayepita kwa sikukuu. Milango yake yote ni tupu, makuhani wake wanaugua, wabinti zake wana huzuni, na muji wenyewe uko katika uchungu. Waadui zake ndio wanaoutawala na wanafanikiwa, maana Yawe ameutesa kwa sababu ya makosa yake mengi. Watoto wake wanapelekwa katika uhamisho. Utukufu wote wa watu wa Sayuni umetoweka; wakubwa wake wamekuwa kama kulungu wasiokuwa na malisho. Waliwakimbia watesi wao bila nguvu. Unapokuwa sasa mabomoko matupu, Yerusalema unakumbuka utukufu wake. Ulipoangukia katika mikono ya waadui zake, hakuna aliyekuwa pale kwa kuusaidia. Washindi wake walichekelea kuanguka kwake. Muji Yerusalema ulitenda zambi kubwa, ukakuwa muchafu kwa ajili ya zambi zake. Wote waliousifia wanauzarau, maana wameuona uchi wake. Muji wenyewe unaugua na kujificha kwa ajili ya haya. Uchafu wake ulionekana waziwazi, lakini muji wenyewe haukujali mwisho wake. Anguko lake lilikuwa kubwa sana; hakuna anayeweza kuufariji. Unasema: Angalia, ee Yawe, mateso yangu, maana adui yangu ameshinda. Waadui wamenyoosha mikono yao, wapate kukamata vitu vyake vyote vya bei kali. Kweli umeona watu wa mataifa wakiingia ndani ya hekalu, watu ambao Yawe aliwakataza kuingia kati kusanyiko lake. Watu wa Yerusalema wote wanaugua, wakitafuta chakula; wanatoa vitu vyao vya bei kali kwa kupata chakula, kusudi wajirudishie nguvu zao. Nao muji unalia, Ee Yawe, uniangalie, ona jinsi nilivyogeuka kuwa zaifu. Enyi wapita njia wote, hivi hamujali kitu? Muangalie, muone kama kuna aliyepatwa na uchungu kama mimi, uchungu Yawe alioniletea siku ya hasira yake kali. Aliteremusha moto kutoka juu, ukanichoma hata ndani ya mifupa yangu. Alinitegea wavu akaninasa, kisha akanirudisha nyuma, akaniacha peke yangu na kuzimia muchana kutwa. Aliyahesabu makosa yangu yote akayakusanya pahali pamoja; aliyafunga katika shingo langu kama nira, nikafyonzwa nguvu zangu kwa uzito wake. Yawe aliniweka katika mikono ya watu ambao siwezi kuwapinga. Yawe aliwakataa waaskari walionilinda, alitangaza wakati kamili wa kuniazibu kuwaponda vijana wangu wanaume. Aliwaponda kama katika kikamulio, watu wangu wa Yuda. Kwa sababu ya hayo ninalia, machozi yananitiririka, sina mutu yeyote wa kunifariji; hakuna yeyote wa kunitia moyo. Watoto wangu wameachwa ukiwa, maana adui yangu amenishinda. Ninainyoosha mikono yangu lakini hakuna wa kunifariji. Yawe ametoa amri juu yangu mimi Yakobo, wajirani zangu wakuwe waadui zangu. Kweli, mimi Yerusalema nimekuwa kitu kichafu kwao. Lakini Yawe amefanya sawa kwa maana nimeliasi neno lake. Munisikilize enyi watu wote, muyaangalie mateso yangu. Wabinti zangu na vijana wangu wanaume wamepelekwa katika utumwa. Niliwaita wapenzi wangu, lakini wao wakanidanganya. Makuhani na wazee wangu wamekufia katika muji, wakijitafutia chakula kusudi wajirudishie nguvu zao. Ona, ee Yawe, ninavyokuwa tabani. Roho yangu imechafuka, moyo wangu unaugua maana nimekuasi vibaya. Kule inje kumejaa mauaji, ndani nako ni kama kifo tu. Sikiliza ninavyolalamika; hakuna wa kunifariji. Waadui zangu wote wamesikia juu ya taabu yangu: wanafurahi kwamba umeniletea hasara. Uifanye ile siku uliyoahidi ifike, uwafanye nao wateseke kama mimi. Uwaazibu kwa ajili ya uovu wao wote. Uwatendee kama ulivyonitendea mimi, kwa sababu ya makosa yangu yote. Ninaugua sana kwa maumivu na moyo wangu unazimia. Kwa hasira yake, Yawe amewaweka watu wa Sayuni katika giza. Ametupa toka mbinguni mpaka katika dunia utukufu wa Israeli. Kwa siku ya hasira yake, alilitupilia mbali hata hekalu lake. Yawe ameharibu bila huruma makao yote ya wazao wa Yakobo. Kwa kasirani yake amevibomoa vikingio vya watu wa Yuda. Ametupa chini na kuchafua ufalme wao na watawala wake. Ameivunja kwa hasira nguvu yote ya Israeli. Hakunyoosha mukono kwa kuwasaidia walipokutana na adui; amewawakia watu wa Yakobo kama moto, akateketeza kila kitu. Amevuta upinde wake kama adui, na kuuweka mukono wake wa kuume tayari, amewaua wote waliopendeza macho. Amemwanga hasira yake kama moto katika hema yetu watu wa Sayuni. Yawe amekuwa kama adui, ameangamiza watu wa Israeli; ameharibu nyumba zake kubwa zote, amevibomoa vikingio vyake. Amewazidishia watu wa Yuda kilio na maombolezo. Amelibomoa hekalu lake kama kibanda katika bustani, ameharibu pahali pake pa kusanyiko. Amefanya sikukuu na siku ya Sabato visahauliwe kule Sayuni, kwa hasira yake kubwa amewakataa mufalme na makuhani. Yawe amechukia mazabahu yake na hekalu lake amelikataa. Amewaachilia waadui wazibomoe kuta za nyumba zake katika muji. Wakapiga kelele ndani ya nyumba ya Yawe kama kelele za wakati wa sikukuu. Yawe alikusudia kuubomoa ukuta wa Sayuni; aliupima na kuhakikisha kila kitu kwamba kimeharibika; minara na kuta za inje ya muji akazifanya ukiwa, zote kwa pamoja zikaangamia. Milango yake imezama ndani ya udongo, ameharibu na kuvunjavunja vifungio vyake. Mufalme na wakubwa wake wako katika uhamisho kati ya mataifa. Hakuna sheria tena, manabii wake hawapati tena maono kutoka kwa Yawe. Wazee wa Sayuni wameikaa chini kimya, wamejitia mavumbi juu ya vichwa na kuvaa gunia. Wabinti wa Yerusalema wameinamisha vichwa chini. Macho yangu yamevimba kwa kulia, roho yangu imechafuka, moyo wangu una huzuni nyingi, kwa sababu ya kuangamizwa kwa watu wangu, kwa sababu watoto wachanga na wale wanaonyonya wanazimia katika barabara za muji. Wanawalilia wamama zao: Chakula kiko wapi, kinywaji kiko wapi? Wanazimia kama wale walioumizwa katika barabara za muji, na kukata roho katika mikono ya wamama zao. Nikuambie nini, ee Yerusalema? Nikulinganishe na nini? Nikufananishe na kitu gani kusudi niweze kukufariji, ee Sayuni uliyekuwa muzuri? Maangamizi yako ni mengi kama bahari, ni nani atakayekuponyesha? Manabii wako wamekuonea maono madanganyifu. Hawakufichua wazi uovu wako kusudi wapate kukurudishia hali yako ya mbele. Lakini walikuonea maono ya uongo na ya kupotosha. Wapita njia wote wanakuchekelea; wanakupigia muunzi, ee Yerusalema, wakitikisa vichwa vyao kwa mazarau na kusema: Huu ndio ule muji uliofikia ukamilifu wa uzuri, muji uliokuwa furaha ya dunia nzima? Waadui zako wote wanakuzomea, wanakupigia muunzi na kukusagia meno, nao wanasema: Tumemwangamiza! Kweli, siku ile tuliyoingojea kwa hamu sasa imefika na tumeiona! Yawe amefanya yale aliyokusudia, ametimiza yale aliyoagiza. Kama alivyopanga tangu kale, ameangamiza bila huruma yoyote. Amewafanya waadui wafurahie azabu yako, amewatukuza mashujaa wa waadui zako. Ee Sayuni, umulilie Yawe! Machozi yatiririke kama muto muchana na usiku! Lia na kuomboleza bila kupumzika! Usiku kucha uamukeamuke na kulia. Umufungulie Yawe yanayokuwa ndani ya moyo wako. Umwinulie mikono yako kwa kuwaombea watoto wako, watoto wanazimia na njaa popote katika barabara. Angalia, ee Yawe, uone! Kuna yeyote uliyemutendea kama ulivyotutendea sisi, hata wamama wawakule watoto wao nao makuhani wauawe ndani ya hekalu lako? Maiti za vijana na wazee zimelala ndani ya mavumbi katika barabara, wabinti na vijana wangu wameuawa kwa upanga; umewaua bila huruma siku ya hasira yako. Umewaalika kama kwenye sikukuu waadui zangu walionitisha kila upande. Katika siku ya hasira yako, ee Yawe, hakuna aliyetoroka au kubakia. Wale niliowazaa na kuwalea, waadui zangu wamewaangamiza. Mimi ni mutu niliyepata mateso kwa fimbo ya kasirani ya Mungu. Amenikamata na kunitembeza katika giza ambako hakuna mwangaza. Amenyoosha mukono wake juu yangu mimi tu, akiniazibu tena na tena muchana kutwa. Amenichakalisha ngozi na nyama, ameivunja mifupa yangu. Amenikusanyia na kunizungushia uchungu na mateso. Amenikalisha katika giza kama watu waliokufa zamani. Amenizungushiia ukuta na siwezi kutoka, amenifunga kwa minyororo mizito. Ingawa ninaita na kuomba musaada anazuiza maombi yangu yasimufikie. Amezifunga njia zangu kwa mawe makubwa, amepotosha mapito yangu. Alikuwa kwangu kama dubu anayevizia, kama simba katika maficho. Alinifukuza katika njia yangu, akanirarua na kuniacha ukiwa. Aliuvuta upinde wake, akanielekezea mushale wake. Alinichoma ndani ya moyo kwa mishale, kutoka katika kifuko chake. Nimekuwa kitu cha kuchekelewa kwa watu wote, muchana kutwa nimekuwa mutu wa kuzomewa. Amenijaza taabu, akanishibisha uchungu. Amenisagisha meno katika mawe, akanifanya nigaegae katika majivu. Moyo wangu haujui tena amani, nimesahau furaha. Nimewaza: Nimekata tamaa kabisa, tumaini langu kwa Yawe limetoweka. Kukumbuka taabu na kutangatanga kwangu kunanipa uchungu na sumu. Ninafikiri juu ya hayo siku zote, nayo roho yangu imejaa huzuni. Lakini ninakumbuka jambo hili moja, nami ninakuwa na tumaini: Wema wa Yawe haukomi, huruma zake hazina mwisho. Uaminifu wake ni mukubwa sana, kila mara kunapokucha ni mupya kabisa. Yawe ndiye sehemu yangu, hivyo nitamuwekea tumaini langu. Yawe ni muzuri kwa wanaomutegemea, kwa wote wanaomutafuta. Ni vizuri kwa mutu kungojea kwa utulivu wokovu unaotoka kwa Yawe. Ni vizuri kwa mutu kujifunza uvumilivu tangu wakati wa ujana wake. Heri kwa mutu kukaa peke yake na kimya, mambo mazito yanapomupata kutoka kwa Mungu. Inamupasa kuinama na kujinyenyekeza, labda tumaini litakuwa likingali. Inamupasa kumugeuzia shavu mwenye kumupiga, na kuwa tayari kupokea matusi yake. Yawe hatatutupilia milele. Ingawa atatufanya tuhuzunike, atakuwa na huruma tena, kadiri ya wingi wa wema wake. Yeye hapendelei kuwatesa wala kuwahuzunisha wanadamu. Wafungwa wote katika inchi wanapoteswa na kupondwa, haki za wanadamu zinapopotoshwa mbele ya Mungu Mukubwa, wanapomunyima mutu haki katika tribinali, basi, Yawe haoni hayo? Nani anayeweza kusema kusudi kitu kifanyike ikiwa Yawe asipoamuru ikuwe hivyo? Maovu na mema yanatokea tu kwa amri ya Mungu Mukubwa. Kwa nini mutu anungunike ikiwa ameazibiwa kwa ajili ya zambi zake? Tupime na kuchunguza mwenendo wetu tupate kumurudilia Yawe. Tumufungulie Mungu mioyo yetu na kumwomba kule juu mbinguni: Tulikukosea na kukuasi, nawe haujatusamehe bado. Umejifunika hasira yako na kutufuatilia, ukatuua bila huruma. Umejifunika wingu kusudi maombi yoyote yasipite. Umetufanya kuwa takataka na uchafu kati ya mataifa. Waadui zetu wote wanatuzomea. Woga na hofu vimetuandama tumepatwa na uharibifu na maangamizi. Macho yangu yanabubujika mito ya machozi kwa sababu ya kuangamizwa kwa watu wangu. Macho yangu yanatelemusha machozi bila kukoma, mpaka Yawe kutoka kule mbinguni aangalie chini na kuona. Ninahuzini sana kuona yale yaliyowapata wabinti wa muji wangu. Nimewindwa kama ndege na hao wanaonichukia bila sababu. Walinitupa ndani ya shimo nikiwa muzima na juu yangu wakalundika mawe. Maji yalianza kunifunika kichwa, nami nikafikiri: Huu ni mwisho wangu. Kutoka chini ndani ya shimo, nilikulilia ee Yawe. Wewe umenisikia nikikulilia: Usiache kusikiliza maombi yangu ya musaada. Nilipokuita ulifika karibu nami ukaniambia: Usiogope! Ulinitetea katika maneno yangu, ee Yawe, uliyakomboa maisha yangu. Uliuona uovu niliotendewa, ee Yawe; uniamulie kwa wema maneno yangu. Umeuona uovu wa waadui zangu, na mipango yao yote juu yangu. Umesikia matukano yao, ee Yawe, na mipango yao yote juu yangu. Maneno na mawazo ya waadui zangu siku nzima, ni juu ya kuniangamiza mimi. Wakiikaa au wakienda, ni mimi ndiye wanayemuzomea. Uwalipize, ee Yawe, sawasawa na matendo yao, sawasawa na kazi ya mikono yao. Uifanye mioyo yao kuwa migumu, na laana yako iwashukie. Uwafuatilie kwa hasira na kuwaangamiza toka katika dunia. Namna gani zahabu yetu ilivyochakaa, zahabu safi kabisa ilivyobadilika! Mawe ya bei kali yamesambazwa kwa barabara zote. Watoto wa Sayuni waliosifiwa sana, waliokuwa na bei kama zahabu safi, namna gani sasa wamekuwa kama vyombo vya udongo, kazi ya mikono ya mufinyanzi! Hata mbweha wanatoa maziwa, na kuwanyonyesha watoto wao; lakini watu wangu wamekuwa wabaya, wanafanya kama mbuni katika jangwa. Midomo ya watoto wachanga imekauka kwa kiu, watoto wanaomba chakula, lakini hakuna anayewapa. Wale waliokula vyakula vinono wanakufa na njaa katika barabara. Waliolelewa na kuvalishwa namna ya kifalme wanafukua kwa mikono kwenye yalala. Kosa la watu wangu lilikuwa kubwa kuliko zambi za watu wa Sodoma, muji ambao uliteketezwa kwa rafla bila kuwa na muda wa kunyoosha mukono. Vijana wa Sayuni walikuwa safi kuliko teluji, walikuwa weupe kuliko maziwa. Miili yao ilikuwa myekundu kuliko mawe ya matumbawe, uso wao kama jiwe la rangi ya samawi. Sasa sura zao ni nyeusi kuliko makaa, wanapita katika barabara bila kujulikana; ngozi yao imebanana na mifupa yao, imekauka, imekuwa kama kuni. Afazali waliouawa kwa upanga kuliko waliokufa kwa njaa, ambao walikufa polepole kwa kukosa mazao ya shamba. Wamama ambao wanakuwa na huruma kubwa, waliwapika watoto wao wenyewe, wakawafanya kuwa chakula chao, wakati watu wangu walipoangamizwa. Yawe ameonyesha kabisa kasirani yake, aliimwanga hasira yake kali, aliwasha moto huko katika Sayuni ambao uliteketeza misingi yake. Wafalme katika dunia hawakuamini wala wakaaji wowote wa ulimwengu, kwamba mwangamizaji na adui wangeweza kuingia katika milango ya Yerusalema. Ni kwa sababu ya zambi za manabii wake na makosa ya makuhani wake, ambao walimwanga damu ya watu wa haki katika muji wake. Walitangatanga katika barabara kama vipofu, walikuwa wamejichafua kwa damu, hata mutu yeyote hangeweza kugusa nguo zao. Watu waliwapigia kelele wakisema: Mutoke, enyi munaokuwa wachafu! Mutoke! Mutoke! Musiguse kitu chochote. Hivyo wakakuwa wakimbizi na kutangatanga; watu wa mataifa walisema: Hawa hawatakaribishwa kukaa kwetu! Yawe mwenyewe aliwatawanya, wala hatawajali tena. Makuhani hawaheshimiwi tena, wazee hawapendelewi tena. Tulichoka kukaa macho kungojea musaada; tulikesha na kungojea kwa hamu taifa ambalo halikuweza kutuokoa. Watu walifuatilia hatua zetu, tukashindwa kupita katika barabara zetu. Mwisho wetu ulikaribia, siku zetu zilitimia, mwisho wetu ulifika. Waliotufuatilia walikuwa wepesi kuliko tai, walitukimbiza kwenye milima walituvizia katika jangwa. Walimunasa yule ambaye maisha yetu yalimutegemea, yule mufalme aliyechaguliwa na Yawe yule ambaye tulisema juu yake: Chini ya ulinzi wake tutaishi kati ya mataifa. Wakaaji wa Edomu, ile inchi ya Uzi, mushangilie na kufurahi kwa sasa. Lakini kikombe hiki cha azabu kitawafikia vilevile. Mutakikunywa na kulewa, hata mutavaa uchi! Azabu ya uovu wako, ewe Sayuni imekamilika; Yawe hatawaacha zaidi katika uhamisho. Lakini ninyi Waedomu atawaazibu kwa uovu wenu, atazifichua zambi zenu. Ukumbuke, ee Yawe, mambo yaliyotupata! Utuangalie, uone haya yetu! Inchi yetu imepewa kwa wageni, nyumba zetu kwa watu wengine. Tumekuwa wayatima, bila baba, wamama zetu ni kama wajane. Maji yetu tunayapata kwa feza, kuni zetu kwa kuzinunua. Tunalazimishwa kufanya kazi kama punda, tumechoka, lakini haturuhusiwi kupumzika. Tumewanyooshea Wamisri na Waasuria mikono, kusudi tupate chakula cha kutosha. Babu zetu walitenda zambi na sasa hawako tena; nasi tunabeba makosa yao. Watumwa wanatutawala, wala hakuna wa kutuokoa toka katika mikono yao. Chakula chetu tunakipata kwa kuhatarisha maisha yetu, maana wauaji wanazungukazunguka katika jangwa. Ngozi zetu zinawaka moto kama furu, kwa sababu ya njaa inayotuchoma. Wanawake wetu wanatendewa kwa kinguvu katika Sayuni, na wabinti wetu katika miji ya Yuda. Wakubwa wetu wametundikwa kwa mikono yao; wazee wetu hawapewi heshima yoyote. Vijana wanalazimishwa kusaga ngano kwa mawe, watoto wanayumbayumba kwa mizigo ya kuni. Wazee wameacha kutoa mashauri yao, vijana wameacha kuimba. Furaha ya mioyo yetu imetoweka, michezo yetu imegeuzwa kuwa maombolezo. Taji tuliojivunia imeanguka. Ole kwetu maana tumetenda zambi! Kwa ajili ya hiyo tumeugua ndani ya moyo, kwa ajili ya hiyo macho yetu yamefifia. Maana mulima Sayuni umeachwa utupu, mbweha wanazungukazunguka humo. Lakini wewe Yawe unatawala milele, kiti chako cha kifalme kinadumu kwa vizazi vyote. Sababu gani umetusahau kwa muda murefu hivyo na kutuacha siku nyingi hivyo? Utugeuze, ee Yawe, kusudi tukurudilie. Uturudishie hali ya zamani. Au, umetukataa kabisa? Umetukasirikia sana? Kwa siku ya tano ya mwezi wa ine, mwaka wa makumi tatu, wakati nilipokuwa katikati ya wale watu waliopelekwa katika uhamisho, karibu na muto Kebari, mbingu zikafunguka, nikapata maono toka kwa Mungu. Katika siku ya tano ya mwezi (ulikuwa mwaka wa tano tangu mufalme Yoyakinu alipopelekwa katika uhamisho katika Babeli), neno la Yawe lilimufikia kuhani Ezekieli mwana wa Buzi, alipokuwa Babeli karibu na muto Kebari. Yawe alinijaza uwezo wake. Nilipoangalia niliona upepo wa zoruba unavuma kutokea upande wa kaskazini: kulikuwa wingu kubwa lililozungukwa na mwangaza, na moto ulitokea humo mufululizo na katikati ya huo moto kulikuwa kitu kinachometameta kama shaba. Kutoka humo nilitambua viumbe vine, ambavyo vilionekana hivi: Vilikuwa na umbo la mwanadamu. Kila kimoja kilikuwa na nyuso ine na mabawa mane. Miguu yao ilikuwa yenye kunyooka; upande wa chini wa miguu yao ulikuwa kama kwato za miguu ya mwana-ngombe, nazo zilimetameta kama shaba safi. Chini ya mabawa yao, kulikuwa mikono inayokuwa sawa ya mutu. Mikono hiyo ilikuwa inaelekea kwenye pande zote ine pamoja na nyuso zao na mabawa yao. Incha za mabawa yao ziligusana kila bawa na bawa lingine. Vilipotembea, vilikwenda mbele moja kwa moja pasipo kugeuka. Juu ya nyuso zao: kila kimoja kilikuwa na uso wa mutu upande wa mbele, uso wa simba upande wa kuume, uso wa ngombe upande wa kushoto, na uso wa tai upande wa nyuma. Mabawa mawili ya kila kimoja yalikuwa yamekunjuliwa juu na kugusana; na kwa mabawa yale mengine mawili, vilifunika miili yao. Popote roho alipotaka kwenda, ndiko vilikwenda; kila kimoja kilikwenda mbele moja kwa moja pasipo kugeuka. Katikati ya vile viumbe kulikuwa kitu kilichoonekana kama mienge ya moto iliyoangaza huku na huku kati ya hivyo viumbe. Moto huo ulikuwa ukiwaka sana na umeme ulitokea humo. Viumbe vile vilikwenda na kurudia mbio kama vile umeme unavyoonekana. Nilipokuwa nikiangalia viumbe vile, nikaona chini karibu na kila kiumbe kulikuwa gurudumu. Magurudumu hayo yalionekana kuwa ya namna moja, yanametameta kama jiwe la zabarajadi na umbo lao lilikuwa kama gurudumu ndani ya gurudumu lingine. Yalipotembea yalikwenda kwa pande zote ine pasipo kugeuka yanapokwenda. Miviringo ya hayo magurudumu ilikuwa mirefu na ya kuogopesha nayo ilikuwa inajaa macho pande zote. Vile viumbe vilipokwenda, magurudumu nayo yalikwenda kandokando yao; na viumbe vile viliponyanyuka juu kutoka kwenye udongo, magurudumu hayo yaliinuka. Popote roho alipokwenda vilikwenda, nayo magurudumu yaliinuka pamoja navyo; maana roho ya hivyo viumbe ilikuwa katika magurudumu hayo. Viumbe hivyo vilipokwenda, magurudumu nayo yalikwenda; viliposimama, nayo yalisimama; vilipoinuka juu kutoka kwenye udongo, magurudumu nayo yaliinuka pamoja navyo. Maana roho wa vile viumbe vya ajabu ilikuwa katika magurudumu hayo. Juu ya vichwa vya vile viumbe kulikuwa kitu kinachofanana na anga, kinangaa kama kioo. Viumbe vile vilisimama chini ya kitu hicho; mabawa mawili ya vile viumbe yalikuwa yamekunjuliwa, moja likielekea lingine, na kwa mabawa mengine mawili vilifunika miili yao. Vilipokuwa vinakwenda, nilisikia sauti ya mabawa yao; sauti ya muvumo huo ilikuwa kama ile ya maji mengi, kama sauti ya ngurumo kutoka kwa Mungu wa majeshi, na kama kelele ya jeshi. Viliposimama, vilikunja mabawa yao. Nilisikia sauti kutoka juu ya kitu kile kinachokuwa kama anga kilichokuwa juu ya vichwa vyao. Juu ya kitu hicho niliona kitu kimoja kinachofanana na kiti cha kifalme chenye rangi la jiwe la yakuti. Juu yake kulikuwa kunaikaa kitu kinachofanana na mutu. Sehemu ya juu ya mwili wake ilingaa kama shaba, nao ulikuwa sawa unazungukwa na moto pande zote. Tokea sehemu ya chini ya mwili wake, niliona kitu kama moto. Mwangaza ulimuzunguka. Ulionekana kama upindi wa mvua wakati wa mvua. Ulionekana kufanana na utukufu wa Yawe. Nilipouona, nilianguka uso mpaka chini, nikasikia sauti ya mutu mwenye kusema. Naye akaniambia: Wewe mwanadamu! Simama. Ninataka kusema nawe. Alipokuwa akisema nami, Roho wa Mungu akaniingia na kunisimamisha wima. Halafu nikamusikia akiniambia hivi: Wewe mwanadamu ninakutuma kwa Waisraeli, taifa la waasi ambao wameniasi. Wameendelea kunikosea mimi mpaka leo sawa vile babu zao walivyofanya. Watu hao ni wenye kichwa nguvu na moyo mugumu. Ninakutuma kwao, nawe utawaambia: “Bwana wetu Yawe anasema hivi.” Wakisikia au wakikataa kusikia, maana hao ni watu waasi, watatambua kwamba nabii yuko katikati yao. Lakini, ewe mwanadamu usiwaogope hao wala maneno yao; maana uko katikati ya michongoma na miiba, nawe unaikaa pamoja na nge; usiogope maneno yao wala usitishwe na nyuso zao, maana hao ni watu waasi. Wewe utawaambia maneno yangu, wakisikia au wakikataa kusikia, maana hao ni watu waasi. Lakini, ewe mwanadamu, usikilize ninayokuambia, wala usikuwe mwasi kama watu hao waasi. Ufungue kinywa chako, ukule ninachokupa. Nilipoangalia, nikaona nimenyooshewa mukono, nao ulikuwa ukishika kitabu kilichozingwa. Basi akakikunjua mbele yangu, nacho kilikuwa kimeandikwa mbele na nyuma maneno ya maombolezo, kilio na hasara. Akaniambia: Wewe mwanadamu, kula unachopewa; kula kizingo hiki cha kitabu, kisha uende kusema na Waisraeli. Kwa hiyo nikafungua kinywa changu, naye akanikulisha kile kitabu. Halafu akaniambia hivi: Wewe mwanadamu, kula kizingo hiki ninachokupa, ujaze tumbo lako na kulishibisha. Basi, nikakikula, nacho kikakuwa kitamu ndani ya kinywa changu kama vile asali. Kisha akaniambia hivi: Wewe mwanadamu, uwaendee Waisraeli, uwaambie maneno yangu. Mimi sikutumi kwa taifa lenye luga ya kigeni na lenye usemi mugumu, lakini kwa Waisraeli. Sikutumi kwa mataifa mengi yenye luga ya kigeni na ngumu ambayo hauifahamu. Hakika ningelikutuma kwa watu kama hao, hakika wao wangekusikiliza. Lakini Waisraeli watakataa kukusikiliza, maana hawataki kunisikiliza mimi. Watu wote wa Israeli ni wenye kichwa nguvu na moyo mugumu. Nimekufanya kuwa mugumu, na kichwa chako kuwa nguvu kwa kupingana nao. Kama vile almasi inavyokuwa ngumu kuliko mawe mengine, ndivyo nilivyokufanya ukuwe na kichwa kigumu. Usiwaogope wala usitishwe na nyuso zao, maana hao ni watu waasi. Tena akaniambia hivi: Wewe mwanadamu, maneno yote nitakayokuambia uyaweke ndani ya moyo wako, na uyasikilize vizuri. Kisha uende kwa watu wako waliopelekwa katika uhamisho, uwaambie kwamba: “Yawe anasema hivi”, wakisikia au wakikataa kusikia. Kisha Roho akaninyanyua juu, nami nikasikia nyuma yangu sauti kama ya tetemeko kubwa ikisema: Utukufu wa Yawe usifiwe mbinguni. Vilevile nilisikia sauti ya mabawa ya vile viumbe yalipokuwa yanagusana, pamoja na sauti ya shindo la yale magurudumu kandokando yao. Basi, Roho akaninyanyua juu na kunipeleka mbali. Yawe alinijaza uwezo wake. Nami nikaenda nikiwa na uchungu na hasira katika roho yangu. Nikawafikia wale watu waliokuwa katika uhamisho, waliokuwa wakiishi karibu na muto Kebari huko Teli-Abibu. Nikakaa nao kwa muda wa siku saba nikishangaa sana. Nyuma ya siku saba, neno la Yawe lilinifikia kusema hivi: Wewe mwanadamu, nimekuweka kuwa mulinzi wa Waisraeli. Utakuwa ukisikiliza maneno ninayokuambia na kwenda kuwatolea maonyo yangu. Nikimwambia mutu mwovu kwamba hakika atakufa, nawe haumwonyi au kumwambia aache mwenendo wake mubaya apate kuyaokoa maisha yake, basi, mutu huyo mwovu atakufa kwa uovu wake; lakini wewe utabeba lazima ya damu yake. Lakini, ukimwonya mutu huyo mwovu naye hauachi uovu wake au mwenendo wake mubaya, mutu huyo atakufa kwa ajili ya uovu wake, lakini wewe utakuwa umeyaokoa maisha yako. Tena, kama mutu wa haki akigeuka katika haki yake na kutenda uovu, nami nikimwekea kikwazo, mutu huyo atakufa. Kwa vile haukumwonya, atakufa kwa sababu ya zambi yake, nayo matendo yake ya haki hayatakumbukwa. Lakini wewe utabeba lazima ya damu yake. Lakini, ukimwonya mutu wa haki asitende zambi, naye akiacha kutenda zambi, hakika mutu huyo ataishi, kwa sababu amepokea maonyo yako, nawe utakuwa umeyaokoa maisha yako. Yawe akanijaza uwezo wake; naye akaniambia: Simama, uende katika bonde nami nitaongea nawe huko. Basi, nikasimama na kwenda katika bonde. Nikiwa huko nikauona utukufu wa Yawe ukiwa umesimama huko kama utukufu ule niliokuwa nimeuona karibu na muto Kebari; nami nikaanguka uso mpaka chini. Lakini roho ya Mungu aliniingia na kunisimamisha wima. Kisha Mungu akaongea nami, akaniambia: Kwenda ujifungie ndani ya nyumba yako. Ewe mwanadamu, utafungwa kwa kamba kusudi usiweze kutoka na kuwaendea watu. Nitaufanya ulimi wako ukuwe muzito nawe utakuwa bubu kusudi usiweze kuwakaripia kwa sababu ni waasi. Lakini wakati nitakaposema nawe nitakifungua kinywa chako, nawe utawaambia kwamba: “Yawe anasema hivi”. Atakayesikia, asikie; atakayekataa kusikia, akatae; maana hao ni watu waasi. Yawe akaniambia tena: Wewe mwanadamu, twaa tofali, uliweke mbele yako na uchape juu yake muji, kama wa Yerusalema. Onyesha kwamba muji ule umeshambuliwa. Utaujengea nafasi za kupandia juu ya kuta zake. Kandokando yake uweke makambi ya waaskari, na gongo ya kubomoa kuta. Nawe utwae bamba la chuma. Ulisimamishe likuwe kama ukuta wa chuma kati yako na muji. Kisha utaelekezea muji huo uso wako nao utashambuliwa na utaushambulia. Hiki kitakuwa kitambulisho kwa taifa la Waisraeli. Kisha, uende ulalie mbavu kwa upande wako wa kushoto. Muda wote utakapokaa katika hali hiyo utabeba uovu wa Waisraeli kama muzigo muzito. Nimekupangia muda wa siku mia tatu na makumi kenda. Muda huu ni sawa na miaka ya azabu yao: siku moja ni sawa na mwaka mumoja. Utabeba azabu ya Waisraeli kwa muda huu. Utakapotimiza siku hizo, utalalia kwa upande wa kuume, na hapo utabeba azabu ya watu wa ufalme wa Yuda kwa muda wa siku makumi ine; nimekupangia siku moja kuwa sawa na mwaka mumoja. Kisha, utauelekea Yerusalema ulioshambuliwa kwa vita na kuunyooshea mukono mutupu na kutabiri juu yake. Nitakufunga kamba kusudi usiweze kugeuka toka upande mumoja mpaka upande mwingine, mpaka wakati kushambuliwa kwa Yerusalema kutakapomalizika. Wewe utwae ngano, shayiri, mahalagi, manjegere, mutama na ulezi, uvitie vyote katika chombo kimoja, ujitengenezee mukate. Mukate huo ndio utakaokuwa chakula chako wakati unapolala kwa upande mumoja, siku zote mia tatu na makumi kenda. Chakula utakachokula kitapimwa, nacho kitakuwa grama mia mbili makumi tatu kwa siku; nawe utakula mara moja tu kwa siku. Maji nayo utayakunywa kwa kipimo: vikombe viwili, mara moja kwa siku. Utatwaa mavi ya mutu, uwashe nayo moto, upike mukate juu yake na kuukula mbele ya watu. Yawe aliniambia: Vile ndivyo Waisraeli watakavyokula mukate wao muchafu wakiwa kati ya mataifa ninakowapeleka. Halafu nikamwambia hivi: Ee, Bwana wangu Yawe, sijajichafua hata kidogo kwa kula nyamafu wala nyama aliyeuawa na nyama wa pori, wala sijapata kuonja nyama anayehesabiwa kuwa muchafu tangu ujana wangu. Kisha akaniambia: Basi, ninakuruhusu utumie mavi ya ngombe pahali pa mavi ya mutu kwa kupika mukate wako. Tena akaniambia hivi: Wewe mwanadamu, mimi nitaharibu akiba ya chakula katika Yerusalema; wakaaji wake watakula chakula watakachopimiwa kwa hofu. Watakunywa maji watakayopimiwa kwa kufazaika. Nitafanya hivyo kusudi wakose chakula na maji, na kila mumoja atamwangalia mwenzake kwa kufazaika; nao watakuwa zaifu kwa ajili ya azabu yao. Yawe aliniambia hivi: Wewe mwanadamu, utwae upanga mukali, uutumie kama wembe wa kinyozi. Unyoe kichwa na ndevu zako. Kisha utwae mizani, upime nywele zako na kuzigawanya kwa sehemu mbalimbali. Kisha kutimia kwa wakati wa kushambuliwa kwa muji wa Yerusalema, utachoma sehemu moja ya tatu ya nywele zako katikati ya muji. Sehemu ingine moja ya tatu utaikatakata kwa upanga ukiuzunguka muji. Sehemu ya tatu ya mwisho utaipeperusha kwa upepo, nami nitauchomoa upanga wangu na kuwafuatilia nyuma. Lakini utatwaa sehemu ndogo tu ya nywele zako na kuifungia kwenye upindo wa nguo yako. Utwae vilevile nywele kidogo uzitupe ndani ya moto na kuziteketeza. Moto utatokea humo na kuteketeza watu wote wa Israeli. Bwana wetu Yawe anasema hivi: Ndivyo itakavyokuwa juu ya Yerusalema. Mimi niliuweka kuwa katikati ya mataifa, umezungukwa na inchi za kigeni pande zote. Lakini wakaaji wake wameyaasi maagizo na masharti yangu, wakakuwa wabaya kuliko mataifa na inchi zinazowazunguka. Kweli, wameyakataa maagizo yangu na kuacha kuyafuata masharti yangu. Kwa hiyo, Bwana wetu Yawe anasema hivi: Ninyi ni waasi kuliko mataifa yanayowazunguka, hamukuishi kulingana na masharti yangu, wala hamukuyashika maagizo yangu, lakini mumetenda kulingana na maagizo ya mataifa yanayowazunguka. Basi, Bwana wetu Yawe anasema hivi: Nitapingana nanyi nami nitatimiza hukumu zangu juu yenu mbele ya mataifa. Kutokana na machukizo yenu yote nitawaazibu kwa azabu ambayo sijapata kuwapa ninyi na ambayo sitairudilia tena. Hukohuko katika muji wazazi watawakula watoto wao wenyewe na watoto watawakula wazazi wao. Nitatimiza hukumu zangu juu yenu na watakaobaki wazima nitawasambaza pande zote. Kwa hiyo, kama vile ninavyoishi, –ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe– kwa vile mumechafua Pahali Patakatifu pangu, kwa matendo yenu mabaya na machukizo yenu, mimi nitawaangamiza bila huruma na bila kumwacha mutu yeyote. Sehemu moja ya tatu ya watu wako, ee Yerusalema, itakufa kwa ugonjwa mukali na kwa njaa. Sehemu ingine moja ya tatu itakufa katika vita. Na sehemu moja ya tatu inayobaki nitaisambaza pande zote za dunia na nitachomoa upanga wangu na kuwafuatilia nyuma. Ndivyo nitakavyomaliza hasira yangu, nami nitakuwa nimetuliza kasirani yangu na kufarijika ndani ya moyo. Hapo ndipo watakapojua kwamba mimi, Yawe, nimewaazibu kwa sababu ya wivu wangu kwa ukosefu wenu wa uaminifu. Tena, wewe Yerusalema nitakufanya kuwa ukiwa na kitu cha kuchekelewa kati ya mataifa yanayokuzunguka na mbele ya watu wote wanaopita karibu nawe. Utakuwa kitu cha kuzarauliwa na cha haya, mufano wa kitu cha kuchukiza kwa makabila yanayokuzunguka, wakati nitakapotimiza hukumu zangu juu yako kwa hasira na kasirani yangu kali. Ni mimi Yawe ninayasema hivyo. Wakati huo nitaiachilia mishale yangu mikali ya njaa iwachome na kuangamiza wakaaji wako. Nitawafanya wakufe na njaa kwa kuiharibu akiba yao ya chakula. Nitakutumia njaa na nyama wakali ambao wataua watoto wako; magonjwa makali, mauaji, na vita itakuja kukuangamiza. Ni mimi, Yawe, ninayesema hivyo. Neno la Yawe lilinifikia kusema hivi: Wewe mwanadamu, uelekeze uso wako kwenye milima ya Israeli, nawe utoe unabii kwa ajili ya wakaaji wake na kusema hivi: Musikilize neno la Bwana wetu Yawe, enyi wakaaji wa milima ya Israeli! Anawaambia ninyi wakaaji wenye kuwa katika milima na vilima na katika maporomoko na mabonde kwamba: Mimi mwenyewe, Bwana wenu Yawe, nitaleta upanga na kuharibu sehemu zenu zote zilizoinuka za kutambikia. Mazabahu zenu zitaharibiwa na pahali penu pa kufukizia ubani patavunjwavunjwa. Wale watakaouawa nitawatupa mbele ya sanamu zenu za miungu. Maiti za Waisraeli nitazilalisha mbele ya sanamu zao za miungu, na mifupa yenu nitaisambaza kandokando ya mazabahu zenu. Pahali pote munapoishi, miji yenu itakuwa ukiwa na sehemu zenu zinazoinuka za kutambikia zitabomolewa, mazabahu zenu zitabomolewa na kuwa ukiwa, sanamu zenu za miungu zitavunjwa na kuharibiwa. Pahali penu pa kufukizia ubani patabomolewa na chochote mulichofanya kitatoweka. Wale watakaouawa wataanguka kati yenu, nanyi mutatambua kwamba mimi ni Yawe. Hata hivyo, nitawaacha wengine wabaki wazima; wamoja kati yenu wataponyoka upanga nao watasambazwa katika inchi mbalimbali. Halafu wale walioponyoka watanikumbuka katikati ya mataifa ambamo watakuwa wamepelekwa katika uhamisho. Nitakuwa nimewavunja moyo wao wa uzinzi ambao ulinitupilia mbali, na macho yao yaliyozini na sanamu zao. Kwa hiyo watajichukia wao wenyewe kwa sababu ya maovu na machukizo yao yote waliyoyatenda. Nao watajua kwamba mimi ni Yawe; sikusema bure kwamba nitawaletea hasara hizo zote. Bwana wetu Yawe akaniambia hivi: Upige mikono, piga kishindo kwa muguu na kusema: Ole kwenu Waisraeli kwa sababu ya machukizo yenu yote; kwa sababu mutakufa kwa upanga, njaa na kwa ugonjwa mukali. Anayekuwa mbali sana atakufa kwa ugonjwa mukali. Anayekuwa karibu atauawa kwa upanga. Atakayekuwa amebaki na kuponyoka hayo mawili atakufa kwa njaa. Ndivyo nitakavyotimiza kasirani yangu juu yao. Wakati maiti zao zitakapokuwa zimelala kati ya sanamu zao za miungu, na kwenye mazabahu zao juu ya kila mulima, chini ya kila muti wenye kivuli, chini ya kila muti wa mwalo wenye majani na popote walipotolea sadaka zenye harufu nzuri ya kuzipendeza sanamu zao za miungu. Nanyi mutatambua kwamba mimi ni Yawe. Nitanyoosha mukono wangu juu yao, na kuiharibu inchi yao. Tangu huko katika jangwa upande wa kusini mpaka katika muji wa Dibla kwa upande wa kaskazini, nitaifanya inchi yao kuwa matongo kabisa wasipate pahali pa kuishi. Nao watatambua kwamba mimi ni Yawe. Neno la Yawe lilinifikia kusema hivi: Wewe mwanadamu, uwaambie wakaaji wa inchi ya Israeli kwamba Bwana wenu Yawe anasema hivi: Ni Mwisho! Mwisho umeifikia inchi yote, kutoka pande zote ine! Sasa mwisho umewafikia; sasa mutausikia ukali wa hasira yangu juu yenu. Nitawahukumu kufuatana na mwenendo wenu. Nitawaazibu kwa ajili ya machukizo yenu yote. Sitawaachilia wala sitawaonea huruma. Nitawaazibu kulingana na mienendo yenu, nayo machukizo yenu yangali bado kati yenu. Halafu mutatambua kwamba mimi ni Yawe. Bwana wetu Yawe anasema hivi: Mutapatwa na hasara! Hasara isiyoonekana bado! Mwisho umekuja! Kweli, mwisho umefika! Umewafikia ninyi! Enyi wakaaji wa inchi hii, maangamizi yenu yamekuja! Wakati umekuja, siku imekaribia. Hiyo ni siku ya makelele na siyo ya sauti za shangwe kwenye mulima. Sasa mutausikia uzito wa hasira yangu juu yenu. Nitawahukumu kulingana na mwenendo wenu; nitawaazibu kufuatana na machukizo yenu. Sitawaachilia wala sitawaonea huruma. Nitawaazibu kulingana na mienendo yenu nayo machukizo yangali bado kati yenu. Halafu mutatambua kwamba ni mimi Yawe ninayewaangamiza. Muangalie, siku ile inakuja! Maangamizi yenu yamekuja. Ubaya uko kila pahali na kiburi kimepanda sana. Mateso makali yanaendelea kuwa mubaya zaidi. Hakuna hata mumoja kati yenu atakayebaki, wala vitu mulivyojilundikia kwa wingi au utajiri wenu; hakutakuwa mutu mwenye heshima kati yenu. Wakati umetimia, ile siku imekaribia. Mununuzi asifurahi wala muchuuzi asiomboleze; kwa sababu kasirani yangu itawaangukia watu wote. Wachuuzi watahomba kabisa hata ikiwa wangali wazima. Kwa maana unabii huu ni juu ya watu wote nao hautavunjwa. Kutokana na uovu wake, mutu hatayaokoa maisha yake. Baragumu imepigwa na kuwafanya wote wakuwe tayari. Lakini hakuna anayekwenda kwa vita, kwa maana kasirani yangu iko juu ya watu wote. Inje kuna kifo kwa upanga na ndani ya muji kuna ugonjwa mukali na njaa. Wanaokuwa katika vijiji watakufa kwa upanga; wanaokuwa katika muji wataangamizwa na njaa na ugonjwa mukali. Ikiwa kuna watu walioponyoka, watakimbilia kwenye milima kama njiwa waliotishwa katika bonde. Kila mumoja wao ataomboleza kwa ajili ya zambi zake. Mikono ya kila mutu itakuwa zaifu na magoti yake yataregea kabisa. Watavaa gunia, hofu itawashika, nao watapata haya na vichwa vyao vyote vitanyolewa. Watatupa feza yao ndani ya barabara na zahabu yao itakuwa kama kitu kichafu. Feza na zahabu zao hazitaweza kuwaokoa katika siku hiyo ya kasirani ya Yawe; wala hawataweza kushiba au kujaza tumbo zao feza na zahabu waliyojilundikia; maana mali hiyo ndiyo iliyosababisha zambi yao. Walijivuna kwa ajili ya vitu vyao vizuri vya mapambo, wakajifanyia sanamu za miungu zinazochukiza, vitu vibaya kabisa. Kwa sababu hiyo nitavifanya kuwa uchafu mbele yao. Utajiri wao nitautia katika mikono ya mataifa mengine; watu waovu wa dunia wataunyanganya na kuuchafua. Nitageuza uso wangu usiwaelekee; nitaachilia hekalu langu lichafuliwe. Wanyanganyi wataingia humo ndani na kulichafua. Tengeneza munyororo; kwa maana inchi imejaa makosa ya umwangaji wa damu na muji umejaa mateso makali. Nitaleta watu wa mataifa mabaya sana nao watarizi nyumba zao. Nitakikomesha kiburi chao, na pahali pao pa kutambikia patachafuliwa. Uchungu mukali utakapowafikia, watatafuta amani, lakini haitapatikana. Watapata hasara kwa mufululizo; nazo habari mbaya zitafuatana. Watamwomba nabii awatabirie. Makuhani hawatakuwa na sheria yoyote; na wazee watakosa shauri la kuwapatia. Mufalme ataomboleza, mukubwa atakata tamaa na watu watatetemeka kwa hofu. Nitawatendea kufuatana na mienendo yao, nitawahukumu kama nilivyowahukumu wengine. Halafu watatambua kwamba mimi ni Yawe. Katika mwaka wa sita, siku ya tano ya mwezi wa sita tangu tulipopelekwa katika uhamisho, nilikuwa nikiikaa ndani ya nyumba yangu pamoja na wazee wa Yuda. Basi, kwa rafla nikajazwa na uwezo wa Yawe. Nilipoangalia, nikaona kitu kilichofanana na mwanadamu. Sehemu yake ya chini, iliyoonekana kama ndio kiuno chake, ilikuwa kama moto. Toka kiuno chake kwenda juu alimetameta kama vile shaba. Basi, akanyoosha kitu kinachokuwa kama vile mukono, akanikamatia kwa nywele zangu. Roho wa Mungu akaninyanyua kati ya dunia na mbingu, akanipeleka mpaka Yerusalema nikiwa katika maono hayo ya Mungu. Nikafika kwenye kiingilio cha mulango wa baraza ya ndani inayoelekea upande wa kaskazini, pahali palipowekwa sanamu iliyomuletea Mungu wivu. Utukufu wa Mungu wa Israeli ulikuwa hapo; nao ulikuwa kama utukufu ule niliouona katika maono kule katika bonde. Kisha Mungu akaniambia: Wewe mwanadamu, angalia upande wa kaskazini. Nami nikaangalia upande wa kaskazini, na huko upande wa kaskazini wa mulango wa mazabahu, niliona ile sanamu iliyomuchukiza Mungu. Basi, Mungu akaniambia hivi: Wewe mwanadamu, unaona mambo wanayofanya, machukizo makubwa Waisraeli wanayofanya kusudi wapate kunifukuza kutoka katika hekalu langu? Tena utaona machukizo mengine makubwa zaidi. Kisha akanipeleka mpaka kwenye mulango wa kuingilia ndani ya uwanja. Nilipoangalia nikaona tundu juu ya ukuta. Naye akaniambia hivi: Wewe mwanadamu, toboa ukuta huu. Nami, nikatoboa, nikaona kulikuwa mulango. Tena akaniambia: Ingia ndani uangalie machukizo mabaya wanayofanya humo. Basi, nikaingia, nikaona vitu vya kuchukiza vimechorwa kuzunguka ukuta: kila aina ya nyama wanaotambaa, vidudu, na sanamu zote za miungu ya Waisraeli. Na mbele yao kulikuwa wazee makumi saba wa taifa la Waisraeli pamoja na Yazania mwana wa Safanu. Kila mumoja alikuwa na chetezo katika mukono, na moshi wa ubani ulipanda juu. Kisha Mungu akaniambia: Wewe mwanadamu, umeona mambo wazee wa Waisraeli wanayotenda kwa uficho, kila mutu katika chumba chake cha sanamu. Wanasema: Yawe hatuoni. Yawe ameiacha inchi. Tena akaniambia: Utaona tena machukizo makubwa zaidi wanayotenda. Kisha akanipeleka mpaka kwenye mulango wa upande wa kaskazini wa nyumba ya Yawe. Huko kulikuwa wanawake wameikaa wakimwombolezea mungu Tamuzi. Mungu akaniambia: Wewe mwanadamu, umeyaona hayo? Utaona tena machukizo mengine makubwa kuliko hayo. Kisha akanipeleka mpaka katika uwanja wa ndani wa nyumba ya Yawe. Huko kwenye mulango wa hekalu, kati ya baraza na mazabahu, kulikuwa wanaume yapata makumi mbili na watano, wakigeuzia mugongo wao upande wa hekalu, na nyuso zao zikielekea upande wa mashariki. Walikuwa wanaabudu jua wakielekea upande wa mashariki. Mungu akaniambia: Wewe mwanadamu, umeyaona mambo hayo? Hata hivyo, watu wa Yuda wanaona machukizo hayo kuwa ni kidogo. Wanajaza mateso makali katika inchi na kuzidi kunikasirikisha. Angalia jinsi wananichukiza! Kwa sababu ya mambo hayo watasikia uzito wa kasirani yangu. Sitamwacha hata mutu mumoja aponyoke wala sitamwonea huruma mutu yeyote. Hata wakinililia kwa sauti kubwa mimi sitawasikiliza. Kisha nikamusikia Yawe akisema kwa sauti kubwa: Mujongee karibu ninyi mutakaouazibu muji huu. Mukuje na silaha zenu za kuangamiza. Watu sita wakakuja kutoka upande wa mulango wa juu unaoelekea upande wa kaskazini, kila mumoja na silaha yake ya kuangamiza katika mukono wake. Pamoja nao, kulikuwa mutu mumoja ambaye alikuwa amevaa nguo ya kitani, naye ana chupa la wino. Wakaingia ndani ya hekalu, wakasimama pembeni ya mazabahu ya shaba. Kisha utukufu wa Mungu wa Israeli uliondoka pale juu ya makerubi na kupanda juu mpaka kwenye kizingiti cha nyumba ya Yawe. Yawe akamwita mutu yule aliyekuwa amevaa nguo ya kitani, mwenye chupa la wino, akamwambia hivi: Pita katikati ya Yerusalema, upate kutia kitambulisho kwenye vipaji vya nyuso za watu wanaohuzunika na kulia kwa sababu ya machukizo yote yanayotendeka katika muji huu. Kisha akawaambia wale wengine mimi nikiwa ninasikia: Mupite katika muji, muue watu; musimwachilie mutu yeyote wala kuwa na huruma. Muwaue wazee palepale, vijana wanaume na wabinti, watoto na wanawake; lakini kila mumoja mwenye kuwa na kitambulisho, musimuguse. Muanzie katika hekalu langu. Basi, wakaanza na wazee waliokuwa mbele ya nyumba ya Yawe. Akawaambia: Muchafue nyumba ya Yawe kwa kuvijaza viwanja vyake maiti, kisha musonge mbele. Basi, wakaenda, wakawaua watu katika muji. Wakati walipokuwa wakiwaua, mimi niliachwa peke yangu, nikaanguka uso mpaka chini, nikalia: Ee Bwana wangu Yawe, utaangamiza watu wote wa Israeli waliobaki, ukitimiza kasirani yako juu ya Yerusalema? Naye akaniambia: Uovu wa Waisraeli na watu wa Yuda ni mukubwa sana. Inchi imejaa umwagaji wa damu na katika muji hakuna haki, kwa maana wanasema: Yawe ameiachilia inchi; Yawe haoni. Kwa upande wangu, sitawaachilia wala kuwahurumia; nitawatendea kufuatana na matendo yao. Kisha mutu yule aliyevaa nguo ya kitani, mwenye chupa la wino, akarudi na kutoa habari hii: Nimefanya kama ulivyoniamuru. Kisha nikaona kwamba katika lile anga juu ya vichwa vya makerubi kulikuwa kitu kinachofanana na jiwe la rangi ya samawi, umbo lake kama kiti cha kifalme. Mungu akamwambia yule mutu aliyevaa nguo ya kitani: Kwenda katikati ya magurudumu yanayokuwa chini ya makerubi, ujaze mikono yako na makaa ya moto unaokuwa katikati yao na kuyasambaza juu ya muji. Nikamwona akienda. Wale makerubi walikuwa wamesimama upande wa kusini wa nyumba ya Yawe, yule mutu alipoingia ndani; wingu likafunika kiwanja cha ndani. Utukufu wa Yawe ukapanda juu tokea wale makerubi ukaenda kwenye kizingiti cha nyumba hiyo, na lile wingu likaijaza nyumba, na kiwanja kilijaa mwangaza wa utukufu wa Yawe. Shindo la mabawa ya makerubi iliweza kusikilika hata kwenye kiwanja cha inje, kama sauti ya Yawe wa majeshi anaposema. Yawe alipomwamuru yule mutu aliyevaa nguo ya kitani atwae moto toka katikati ya magurudumu yaliyokuwa chini ya makerubi, yule mutu alikwenda na kusimama pembeni ya gurudumu moja. Kerubi mumoja akanyoosha mukono wake kwa kutwaa moto uliokuwa katikati ya makerubi, akatwaa sehemu yake na kuutia katika mikono ya yule mutu aliyevaa nguo ya kitani; naye alipoupokea, akajiendea. Makerubi hao walionekana kuwa na kitu kama mukono wa mutu chini ya mabawa yao. Niliangalia, nikaona kulikuwa magurudumu mane, gurudumu moja pembeni ya kila kerubi. Magurudumu hayo yalimetameta kama jiwe la zabarajadi. Yote mane yalionekana kuwa ya namna moja, na kila gurudumu lilionekana kama liko ndani ya gurudumu lingine. Yaliweza kwenda pande zote bila kugeuka; kule gurudumu la kwanza lilielekea, yote yalifuata. Miili ya hao makerubi, migongo yao, mikono na mabawa yao, pamoja na magurudumu, vyote vilijaa macho pande zote. Niliambiwa kwamba magurudumu yale yanaitwa “Magurudumu Yanayozunguka”. Kila kerubi alikuwa na nyuso ine: uso wa kwanza ulikuwa wa kerubi, uso wa pili ulikuwa wa mwanadamu, uso wa tatu ulikuwa wa simba na uso wa ine ulikuwa wa tai. Makerubi wakanyanyuka juu. Hawa ndio vile viumbe niliowaona karibu na muto Kebari. Makerubi wale walipokwenda, magurudumu nayo yalikwenda pembeni yao. Walipokunjua mabawa yao kusudi wapande juu, magurudumu nayo yalikwenda pamoja nao. Waliposimama, magurudumu nayo yalisimama; hao walipopanda juu, magurudumu nayo yalipanda pamoja nao. Maana roho wa hao viumbe ilikuwa katika magurudumu hayo. Kisha utukufu wa Yawe ulitoka kwenye kizingiti cha nyumba, ukaenda na kusimama juu ya wale makerubi. Makerubi wakakunjua mabawa yao, wakapanda juu, mimi nikiwa ninawaona na yale magurudumu yalikuwa pembeni yao. Wakasimama mbele ya mulango wa upande wa mashariki wa nyumba ya Yawe, na utukufu wa Mungu wa Israeli ulikuwa juu yao. Hawa walikuwa wale viumbe niliowaona chini ya Mungu wa Israeli karibu na muto Kebari, nami nikatambua kwamba ni makerubi. Kila mumoja wao alikuwa na nyuso ine na mabawa mane na chini ya kila bawa kulikuwa kitu kinachokuwa kama mukono wa mutu. Vilevile nilizitambua nyuso zao: zilikuwa zilezile nilizokuwa nimeziona kule kwenye muto Kebari. Kila kiumbe kilikwenda mbele, moja kwa moja. Roho wa Mungu akaninyanyua na kunipeleka mpaka kwenye mulango wa upande wa mashariki wa nyumba ya Yawe. Huko nikawaona watu makumi mbili na watano. Kati yao kulikuwa Yazania mwana wa Azuri na Pelatia mwana wa Benaya, ambao ni wakubwa wa Waisraeli. Yawe akaniambia: Wewe mwanadamu, hawa ndio watu wanaofanya mipango ya uovu na kutoa mashauri mabaya katika muji huu. Wanasema hivi: Wakati wa kujenga nyumba haujakaribia bado. Muji ni kama chungu kikubwa, na sisi ni kama nyama. Kwa hiyo, utoe unabii juu yao! Tabiri ewe mwanadamu! Kisha Roho wa Yawe akaniingia, naye akaniambia: Uwaambie watu kwamba: Yawe anasema hivi: Ni hivi ndivyo munavyosema, enyi Waisraeli. Ninajua mambo munayofikiri juu yake ndani ya moyo wenu. Ninyi mumewaua watu wengi katika muji huu, na kujaza barabara zake na watu waliouawa. Kwa hiyo, Bwana wetu Yawe anasema hivi: Kweli, muji huu ni chungu, na wale waliouawa ndio nyama. Ninyi lazima mutaondolewa katika muji. Ninyi mumeogopa upanga? Basi, mimi nitaleta upanga juu yenu! –Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe.– Nitawatoa ndani ya muji na kuwatoa katika mikono ya watu wa mataifa mengine, nami nitawahukumu. Mutauawa kwa upanga, nami nitawahukumu katika inchi ya Waisraeli. Halafu mutatambua kwamba mimi ni Yawe. Muji Yerusalema hautakuwa tena chungu chenu wala ninyi hamutakuwa nyama ndani yake. Mimi nitawahukumu katika inchi ya Waisraeli. Nanyi mutatambua kwamba mimi ni Yawe ambaye hamukufuata masharti yake na maagizo yake hamukuyatimiza, lakini mumetenda kufuatana na maagizo ya mataifa yanayowazunguka. Nilipokuwa ninatabiri, Pelatia mwana wa Benaya akakufa. Nami nikaanguka uso mpaka chini, nikalia kwa sauti kubwa, nikisema: Ee Bwana Yawe, utawamaliza kabisa Waisraeli waliobaki? Neno la Yawe lilinifikia kusema hivi: Wewe mwanadamu, wandugu zako na wakaaji wa Yerusalema ambao vilevile ni wandugu zako wanasema juu yako na juu ya watu wote wa Israeli wanaokuwa katika uhamisho hivi: Ninyi munaokuwa katika uhamisho muko mbali sana na Yawe; maana Yawe ametupatia sisi inchi hii ikuwe mali yetu. Lakini, uwaambie hao wanaokuwa katika uhamisho kwamba Bwana wao Yawe anasema hivi: Ingawa nimewapeleka mbali kati ya mataifa na kuwasambaza katika inchi zingine, hata hivyo, mimi nipo pamoja nao huko wanakokuwa, kama vile hekalu kwao. Basi, Bwana wetu Yawe anasema hivi: Nitawakusanya toka kati ya watu, nitawakusanya kutoka katika inchi ambako mulisambazwa. Nitawarudisha katika inchi ya Israeli. Nanyi mutakaporudi katika inchi yenu nitaondoa vitu vyote vichafu na machukizo yote. Nitawapa moyo mupya na kuweka roho mupya ndani yenu. Nitauondoa ule moyo mugumu kama jiwe na kuwapa moyo musikilivu, kusudi mupate kufuata masharti yangu na kuyatii maagizo yangu; nanyi mutakuwa watu wangu nami nitakuwa Mungu wenu. Lakini hao ambao moyo wao umeambatana na vitu vichafu na machukizo yao, nitawaazibu kadiri ya mienendo yao. –Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe. Halafu wale makerubi waliyakunjua mabawa yao na kuanza kuruka pamoja na yale magurudumu yaliyokuwa pembeni yao, nao utukufu wa Mungu wa Israeli ulikuwa juu yao. Basi, utukufu wa Yawe ukapanda juu kutoka katikati ya muji, ukasimama juu ya mulima unaokuwa upande wa mashariki wa muji. Nikiwa katika maono hayo, Roho wa Mungu alininyanyua na kunipeleka mpaka katika inchi ya Babeli, kwa watu wanaokuwa kule katika uhamisho. Kisha maono hayo yakatoweka. Hapo nikawaelezea wale waliokuwa katika uhamisho mambo yote Yawe aliyonionyesha. Neno la Yawe lilinifikia kusema hivi: Wewe mwanadamu! Wewe unakaa kati ya watu waasi. Wana macho lakini hawaoni; wana masikio lakini hawasikii. Wao ni watu waasi. Basi, ewe mwanadamu, ufanye kama vile unakwenda katika uhamisho: ondoka muchana wakati wanapokuwa wakikuona, ukimbilie pahali pengine. Kwenda na muzigo wako kama mukimbizi kutoka pahali unapokuwa mpaka pahali pengine wao wakikuona. Labda wataelewa, ingawa wao ni waasi. Utaondoka na muzigo wako kwa wakati wa muchana, waziwazi, mbele ya macho yao. Uondoke magaribi kama vile watu wanaokwenda katika uhamisho wanavyofanya. Wakiwa wanakuangalia toboa ukuta wa nyumba, upitie hapo na kwenda inje. Wakiwa wanakuona, ujibebeshe muzigo wako kwenye mabega na kuondoka wakati wa giza. Funika uso wako usiweze kuona unakwenda wapi. Ndivyo ninavyokufanya kuwa kitambulisho kwa Waisraeli. Basi, nikafanya kama nilivyoamriwa. Siku hiyo, wakati wa muchana, nikafunga muzigo wangu kama muzigo wa mutu anayekimbia. Magaribi nikatoboa ukuta na giza lilipokuwa likiingia, nikatoka, nikibeba muzigo wangu juu ya mabega, watu wote wakiniona. Kesho yake asubui, neno la Yawe lilinifikia kusema hivi: Wewe mwanadamu! Hao waasi Waisraeli hawajakuuliza maana ya kitendo ulichofanya? Uwaambie: Bwana wetu Yawe anasema hivi: Neno langu hili linaelekea mambo yatakayomupata mutawala wa Yerusalema na Waisraeli wote wanaoishi humo. Uwaambie kwamba wewe ni kitambulisho kwao; kama ulivyofanya ndivyo itakavyotendeka kwao: watakwenda katika uhamisho; watakamatwa mateka. Naye mutawala wao atabeba muzigo wake juu ya mabega wakati wa usiku, atatoka kupitia ukuta atakaotoboa apate kutoka; atafunika uso wake kusudi asiione inchi kwa macho yake. Lakini nitatandaza wavu wangu juu yake, naye atanaswa katika mutego wangu. Nitamupeleka Babeli, inchi ya Wakaldea; naye akiwa huko atakufa bila kuiona inchi hiyo. Wafuasi wake wote, washauri wake na waaskari wake wote, nitawasambaza inje kila upande. Nitauchomoa upanga na kuwafuatilia nyuma. Nitakapowasambaza kati ya mataifa mengine na inchi za mbali, halafu watatambua kwamba mimi ni Yawe. Lakini nitawaacha wachache waepuke vita, njaa na ugonjwa mukali; kusudi hao waweze kuwaelezea watu wa mataifa wanamoishi jinsi walivyotenda mabaya. Halafu watatambua kwamba mimi ni Yawe. Neno la Yawe lilinifikia kusema hivi: Wewe mwanadamu, kula chakula na kunywa maji yako ukitetemeka kwa hofu. Uwaambie watu wa inchi hii: Bwana wetu Yawe anasema hivi juu ya wakaaji wa Yerusalema ambao wangali bado katika inchi ya Waisraeli: Watakula chakula chao kwa hofu na kunywa maji yao kwa kufazaika, maana inchi yao haitakuwa na kitu, kwa sababu kila mukaaji ni mutesaji mukali. Miji yenye watu itateketezwa, na inchi itakuwa ukiwa. Nanyi mutatambua kwamba mimi ni Yawe. Neno la Yawe lilinifikia kusema hivi: Wewe mwanadamu: Kwa nini mezali hii inatajwa katika inchi ya Waisraeli: Siku zinakuja na kupita, lakini maono ya nabii hayatimii? Uwaambie kwamba Bwana wetu Yawe anasema kwamba nitakomesha mezali hiyo nao hawataitumia tena katika inchi ya Waisraeli. Uwaambie kwamba wakati umefika ambapo maono yote yatatimia. Maana hakutakuwa tena maono ya uongo au uaguzi kati ya Waisraeli. Mimi Yawe mwenyewe nitatangaza yatakayotukia. Nayo yatatukia bila kukawia. Wakati ninyi mungali munaishi, enyi watu waasi, neno nitakalosema nitalitimiza. –Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe. Neno la Yawe lilinifikia kusema hivi: Wewe mwanadamu, Waisraeli wanafikiri kwamba maono yako yanahusu siku za nyuma sana, na unabii wako unahusu nyakati za mbali sana! Kwa hiyo uwaambie kwamba: Bwana wetu Yawe anasema hivi: Maneno yangu yote yatatimia sasa hivi. –Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe. Neno la Yawe lilinifikia kusema hivi: Wewe mwanadamu, uwakaripie manabii wa Waisraeli wanaotangaza mambo ambayo wameyafikiria wao wenyewe. Uwaambie: Musikilize neno la Yawe! Bwana wetu Yawe anasema hivi: Ole kwenu manabii wapumbafu munaofuata mawazo yenu wenyewe na maono yenu wenyewe! Manabii wenu, enyi Waisraeli ni kama mbweha wanaopitapita katika mabomoko. Hawakwenda kulinda sehemu zile za kuta zilizobomoka wala hawajengi kuta mupya kusudi Waisraeli waweze kujilinda wakati wa vita siku ile ambayo mimi Yawe nimeiweka. Maono yao ni ya uongo mutupu na wanachotabiri ni udanganyifu mutupu. Wanasema “Ni ujumbe wa Yawe” lakini Yawe hakuwatuma; kisha wanamutazamia atimize yale wanayosema. Basi, ninawauliza: Maono yenu si uongo mutupu na utabiri wenu udanganyifu wakati munaposema “Ni ujumbe wa Yawe”, ijapokuwa mimi sijaongea nanyi hata kidogo? Basi, Bwana wetu Yawe anasema hivi: Kwa kuwa maneno yenu ni udanganyifu na maono yenu ni ya uongo mutupu, basi, mimi nitapingana nanyi. –Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe! Nitanyoosha mukono wangu juu yenu ninyi manabii munaotoa maono ya uongo na kutabiri udanganyifu mutupu. Watu wangu watakapokutanika kwa kuamua maneno, ninyi hamutakuwa pale. Wala hamutakuwa katika kitabu cha majina ya Waisraeli na hamutaingia katika inchi ya Waisraeli; halafu mutatambua kwamba mimi ni Bwana wenu Yawe. Manabii hao wanawapotosha watu wangu na kuwaambia “Kuna amani”, wakati hakuna amani. Watu wangu wanajenga ukuta usiofaa, nao wanaupakaa chokaa! Sasa uwaambie hao manabii wanaopakaa chokaa ukuta huo kwamba kutanyesha mvua kubwa ya mawe na zoruba itavuma na ukuta huo utaanguka. Utakapoanguka, watu hawatawauliza hivi: Na ile chokaa mulioupakaa iko wapi? Kwa hiyo Bwana wetu Yawe anasema: Kwa kasirani yangu nitazusha upepo wa zoruba na mvua nyingi ya mawe, navyo vitauangusha ukuta huo. Nitaubomoa kabisa huo ukuta mulioupakaa chokaa, na musingi wake utakuwa wazi. Ukuta huo ukianguka, mutaangamia chini yake. Halafu mutatambua kwamba mimi ni Yawe. Hasira yangu yote nitaimalizia juu ya ukuta huo na juu ya hao walioupakaa chokaa. Nanyi mutaambiwa: Ukuta haupo tena, wala walioupakaa rangi hawapo; huo ndio mwisho wa manabii wa Waisraeli waliotabiri mema juu ya Yerusalema na kuona maono ya amani ijapokuwa hakuna amani. Ni Bwana wetu Yawe anayesema hivyo. Na sasa, ewe mwanadamu, uwaelekee wanawake wa taifa lako ambao wanatabiri mambo ambayo wameyawaza wao wenyewe. Utabiri juu yao na kuwaambia kwamba Bwana wetu Yawe anasema hivi: Ole kwenu ninyi wanawake munaoshona vitepe vyenye hirizi ambavyo kila mutu anavivaa kwenye maunganio ya mikono na kutengeneza vitambaa vyenye hirizi za kila kimo kwa ajili ya watu wa kila umri. Munapowinda maisha ya watu wangu munazani kwamba mutaokoa maisha yenu wenyewe? Mumenizaraulisha mbele ya watu wangu kusudi mupate vitanga vya shayiri na chakula kidogo. Munawaua watu wasiostahili kufa na kuwaacha wazima wanaostahili kuuawa, kwa uongo wenu munaowaambia watu wangu, nao wanawaaminia. Basi, Bwana wetu Yawe anasema hivi: Nitashambulia hirizi zenu munazowafunga nazo watu; nitazipasuapasua toka katika mikono yenu na kuwaacha huru hao munaowawinda kama ndege. Nitavirarua vitambaa vyenu na kuwaokoa watu wangu toka katika mikono yenu; nao hawatakuwa tena kama nyama wa kuwindwa katika mikono yenu. Halafu mutatambua kwamba mimi ni Yawe. Kwa sababu mumewavunja watu wa haki moyo kwa kusema uongo, ijapokuwa mimi sikuwavunja moyo, mukawaimarisha waovu wasiache mienendo yao mibaya na kuokoa maisha yao, basi, ninyi hamutapata tena maono madanganyifu, wala hamutatabiri tena. Nitawaokoa watu wangu toka katika mikono yenu. Halafu mutatambua kwamba mimi ni Yawe. Siku moja wakubwa wamoja wa Waisraeli walinitembelea kwa kutaka shauri. Basi neno la Yawe lilinifikia kusema hivi: Wewe mwanadamu, watu hawa wamekubali mioyo yao itawaliwe na sanamu za miungu; miungu hiyo inawasukuma kutenda zambi. Nitakubali kuulizwa shauri nao? Basi, sema nao uwaambie kwamba Bwana wao Yawe anasema: Mutu yeyote kati ya Waisraeli anayekubali sanamu za miungu zimutawale ndani ya moyo, na kuiruhusu miungu hiyo kumusukuma kutenda zambi, kisha akuje kumwomba nabii shauri, atapata jibu toka kwangu ambalo litafalia hata kwa sanamu zake nyingi za miungu. Mimi Yawe nitaigusa mioyo ya Waisraeli kusudi wanirudilie, maana wamejitenga mbali nami kwa kuabudu sanamu zao za miungu. Basi, uwaambie Waisraeli kwamba: Bwana wetu Yawe anasema hivi: Munirudilie, na kuacha kuziabudu sanamu zenu za miungu. Muache kufanya machukizo. Wakati wowote mutu mumoja kati ya Waisraeli au mugeni yeyote anayekaa katika inchi ya Waisraeli, anapojitenga nami na kuanza kuziabudu sanamu za miungu kwa bidii na zambi hiyo ikiwa kizuizi kati yangu naye, halafu akimwendea nabii kusudi ajue mapenzi yangu, basi, mimi Yawe mwenyewe, nitamujibu mutu yule. Nitapingana naye. Nitamufanya kuwa kitambulisho na mufano; nitamwondoa kabisa kutoka taifa langu. Halafu mutatambua kwamba mimi ni Yawe. Na ikiwa nabii yule akidanganyika na kusema kitu, basi mimi Yawe nimemupotosha. Nami nitanyoosha mukono wangu kwa kumwondoa nabii yule kutoka kwa watu wangu Waisraeli. Nitamwazibu yule nabii pamoja na yule mutu aliyekuja kumwuliza mapenzi yangu; wote watapata azabu ileile. Kwa hiyo Waisraeli hawataniacha tena na kujichafua wenyewe kwa kutenda zambi; kusudi wakuwe watu wangu nami nikuwe Mungu wao. –Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe. Neno la Yawe lilinifikia kusema hivi: Wewe mwanadamu! Taifa fulani likitenda zambi kwa kukosa uaminifu kwangu, mimi nitanyoosha mukono wangu kwa kuliazibu. Nitaiharibu akiba yake ya chakula na kuliletea njaa. Nitawaua watu na nyama wake. Hata kama Noa, Danieli na Yobu wangalikuwa ndani ya inchi ile, wangeyaokoa tu maisha yao wenyewe kwa ajili ya haki yao. –Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe.– Tena nitatuma nyama wa pori katika inchi hiyo na kuwanyanganya watoto wao na kuifanya inchi hiyo kuwa ukiwa, hata hakuna mutu yeyote atakayeweza kupita katika inchi ile kwa sababu ya nyama wakali. Hata kama hao watu watatu wangalikuwa ndani ya inchi ile, kama vile ninavyoishi, –ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe– hawangeweza kuwaokoa hata wana au wabinti zao. Wao wenyewe tu wangeokolewa, lakini inchi ile ingekuwa ukiwa. Tena nitaleta vita juu ya inchi ile na kuamuru waiangamize na kuua watu na nyama wanaokuwa ndani yake. Hata kama hao watu watatu wangalikuwa ndani ya inchi ile, kama vile ninavyoishi, –ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe– hawangeweza kuwaokoa hata wana au wabinti zao. Wao wenyewe tu wangeokolewa. Tena nitaleta ugonjwa mukali katika inchi ile na kwa kasirani yangu nitawaua watu na nyama. Na hata kama Noa, Daneli na Yobu wangelikuwa ndani ya inchi ile, kama vile ninavyoishi, –ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe– hawangeweza kuwaokoa hata mwana au binti. Wangeyaokoa tu maisha yao wenyewe kwa ajili ya haki yao. Lakini Bwana wetu Yawe anasema: Tena nitauazibu Yerusalema kwa mapigo yangu mane ya hukumu kali: vita, njaa, nyama wakali na ugonjwa mukali, nipate kuangamiza watu na nyama ndani yake! Hata hivyo, kutabaki wazima watu watakaoponyoka na kuwaleta wana na wabinti zao kwako, wewe Ezekieli. Utaona jinsi wanavyokuwa waovu sana; nawe utakubali kwamba azabu yangu juu ya Yerusalema ni ya haki. Mienendo na matendo yao vitakuhakikishia kwamba hasara niliyouletea muji huo sikuileta bila sababu. Ni mimi Yawe ninayesema hivyo. Neno la Yawe lilinifikia kusema hivi: Wewe mwanadamu! Muti wa muzabibu ni bora kuliko miti mingine ya pori? Muti wake unafaa kwa kutengeneza kitu chochote? Watu wanaweza kuutumia kwa kutengeneza misumari ya kutundika vitu? Huo unafaa tu kwa kukonga moto. Tena moto unapoteketeza sehemu yake ya mwanzo na ya mwisho na kuikausha sehemu ya katikati, hiyo inafaa kwa kitu chochote? Ulipokuwa haujachomwa ulikuwa haufai kitu, kefu sasa unapokwisha kuchomwa kwa moto na kuwa makaa! Haufai kitu kabisa. Basi, Bwana wetu Yawe anasema hivi: Kama vile nilivyoutoa muti wa muzabibu kati ya miti ya pori kuwa kuni za kukonga moto, ndivyo nilivyotoa wakaaji wa Yerusalema. Nitawaazibu vikali. Hata kama wataukimbia moto, huo moto utawateketeza. Hapo nitakapowaazibu vikali, halafu mutatambua kwamba mimi ni Yawe. Kwa sababu wamekosa uaminifu kwangu, nitaifanya inchi yao kuwa ukiwa. –Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe. Neno la Yawe lilinifikia kusema hivi: Wewe mwanadamu, ujulishe Yerusalema machukizo yake. Uuambie kwamba Bwana wake Yawe anauambia hivi: Kwa asili wewe ulizaliwa katika inchi ya Kanana. Baba yako alikuwa Mwamori, na mama yako alikuwa Muhiti. Siku ile ulipozaliwa, kitofu chako hakikukatwa wala haukusafishwa na maji; haukupakaliwa chumvi wala kuvalishwa nguo za kitoto. Hakuna aliyekuonea huruma na kukufanyia mambo hayo. Hakuna aliyekupenda. Lakini, siku ile ulipozaliwa, ulitupwa huko katika pori kwa sababu siku ulipozaliwa ulichukiza sana. Mimi nilipopita karibu nawe, nikakuona ukigaagaa katika damu yako, nikakuambia: Uishi, na ukomae kama mumea katika shamba. Nawe ukakomaa na kurefuka hata ukakuwa binti. Maziba yako yakakomaa na nywele zako nazo zikarefuka. Lakini ulikuwa uchi kabisa. Nilipopita tena karibu nawe, nikakuona. Wakati huu, ulikuwa umefikia umri wa kupendwa kama binti. Nikalitandaza vazi langu juu yako na kuufunika uchi wako. Nikafanya nawe agano la ndoa, nawe ukakuwa wangu. –Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe. Kisha nikatwaa maji, nikakukogesha kwa kusafisha damu uliyokuwa nayo, nikakupakaa mafuta. Nilikuvalisha vilevile nguo iliyopambwa vizuri na viatu vya ngozi nzuri. Nikakuvalisha mukaba wa kitani safi na kitambaa cha hariri. Nikakupamba kwa mapambo, nikakuvalisha vikomo kwa mikono yako na mukufu kwenye shingo. Nikakutia pete kwenye pua, visikio kwenye masikio yako na juu ya kichwa chako nikakupamba kwa taji nzuri. Basi, ukapambwa kwa zahabu na feza. Nguo yako ikakuwa ya kitani safi na hariri, nayo ilikuwa imepambwa. Ulitumia unga safi, asali na mafuta kwa chakula chako. Ukakuwa na sura nzuri sana, ukaifikia hali ya malkia. Sifa zako zikaenea kati ya mataifa kutokana na uzuri wako, maana uzuri wako ulikamilika kwa sababu ya utukufu niliokujalia. –Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe.– Lakini, ulitegemea uzuri wako, ukatumia sifa yako kwa kufanya uzinzi, ukifanya ukahaba na mutu yeyote anayepita. Ulitwaa sehemu ya nguo zako, ukaitumia kwa kupamba pahali pako pa kutambikia na hapo ndipo ukafanyia uzinzi wako. Jambo la namna hiyo halijapata kutokea wala halitatokea hata kidogo! Ulitwaa vile vitu vyako vizuri vya zahabu na feza nilivyokupa kwa kujipamba, ukajifanyia sanamu za wanaume upate kufanya uzinzi nazo. Ukatwaa nguo nilizokupa zilizopambwa na kuzifunika zile sanamu, na mafuta yangu na ubani wangu, ukavitolea sanamu hizo. Niliwakulisha ninyi kwa unga safi, mafuta na asali. Lakini chakula changu nilichokupa, ulikitoa kwa sanamu hizo kuwa harufu ya kupendeza. –Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe. Tena, wana wako na wabinti zako ulionizalia uliwatwaa, ukawatambikia kwa sanamu zako wapate kukuliwa. Unazani uzinzi wako ulikuwa ni jambo dogo? Jambo hili la kuwachinja watoto wangu kwa kuwa sadaka ya kuteketeza kwa ajili ya sanamu zako ni jambo dogo? Katika machukizo yako yote pamoja na uzinzi wako haukuzikumbuka siku za utoto wako, wakati ulipokuwa uchi kabisa, bila kitu, ukigaagaa katika damu yako! Ole kwako, ole kwako Yerusalema! –Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe.– Kisha kufanya hayo yote ulijijengea nafasi zinazoinuka kila pahali. Kwa mwanzo wa kila barabara ulijijengea nafasi inayoinuka, ukautumia uzuri wako kwa kufanya uzinzi ukijitoa kwa kila mupita njia na kuongeza uzinzi wako. Tena ulifanya uzinzi na jirani zako Wamisri waliojaa tamaa, ukaongeza uzinzi wako na kuichochea hasira yangu. Basi, niliunyoosha mukono wangu kwa kukuazibu. Nilipunguza chakula chako, nikakuachilia kwa waadui zako, wabinti za Wafilistini ambao walipata haya sana juu ya tabia yako chafu sana. Kwa sababu haukutosheka, ulifanya tena uzinzi na Waasuria. Na hiyo vilevile haikukutoshelea. Ulijitoa wewe mwenyewe utumiwe na Wababeli, watu wanaofanya biashara! Hata hivyo haukutosheka. Kweli wewe ni mugonjwa wa mapenzi. –Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe.– Unafanya uzinzi bila kuona haya hata kidogo. Umejijengea nafasi yako yenye kuinuka kwa mwanzo wa kila barabara na kujijengea pahali pa kutambikia katika kila kiwanja. Tena wewe haukukuwa kama kahaba maana ulikataa kulipwa. Ulikuwa kama muke muzinzi anayekaribisha wageni pahali pa mume wake. Kwa kawaida wanaume wanawalipa makahaba, lakini wewe umewalipa wapenzi wako wote, ukiwahonga wakuje kwako toka pande zote upate kuzini nao. Katika ukahaba wako haukufanya kama wanawake wengine: hakuna aliyekubembeleza kusudi uzini naye lakini wewe ulilipa feza pahali pa kulipwa. Sasa basi, ewe kahaba, usikilize neno la Yawe. Bwana wenu Yawe anasema hivi: Wewe umeponda feza, umefunua uchi wako kwa kuzini na wapenzi wako, umeziabudu sanamu zako zote za miungu na kuzitolea damu ya watoto wako. Basi, mimi nitawakusanya wapenzi wako wote uliojifurahisha nao, wote uliowapenda na wote uliowachukia. Nitawakusanya toka pande zote wakushambulie. Nitawafunulia uchi wako wapate kuuona. Nitakuhukumu kama vile wanawake wanaovunja ahadi ya ndoa au wauaji wanavyohukumiwa; nitakuhukumu kwa azabu ya kifo kwa hasira na kwa ajili ya wivu. Nitakutia katika mikono ya wapenzi wako, nao watabomoa nafasi yako yenye kuinuka na pahali pako pa kutambikia. Watakutosha nguo yako na kukunyanganya vitu vyako vya kujipamba, wakuache uchi, bila kitu. Watakuletea kundi kubwa kwa kukushambulia; watakuua kwa kukupiga mawe na kisha watakukatakata kwa panga zao. Nyumba zako wataziteketeza kwa moto na kuwafanya wanawake wengi waone azabu yako. Utakoma kujitoa kwa mutu yeyote afanye uzinzi nawe. Hivi, kasirani yangu itatosheka juu yako, wivu niliokuwa nao juu yako utakwisha; nitatulia wala sitaona hasira tena. Wewe umesahau yale ambayo mimi nilikufanyia ulipokuwa kijana. Wewe umenichukiza sana kwa mambo yale yote. Basi, nitakulipiza kisasi juu ya kila kitu ulichotenda. –Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe.– Haukuongeza uchafu juu ya machukizo yako yote? Ewe Yerusalema! Mutu akitaka kutumia mezali juu yako atasema hivi: Kama vile mama anavyokuwa ndivyo binti wake anavyokuwa. Kweli wewe ni mutoto wa mama aliyemuchukia mume wake na watoto wake; wewe ni sawa na dada zako waliowachukia waume wao na watoto wao. Mama yako alikuwa Muhiti na baba yako alikuwa Mwamori. Dada yako mukubwa ni Samaria, aliyekaa upande wako wa kaskazini pamoja na wabinti zake. Dada yako mudogo ni Sodoma, aliyekaa upande wako wa kusini pamoja na wabinti zake. Lakini wewe haukutosheka kufuata mienendo yao au kutenda sawa na machukizo yao. Kwa muda mufupi tu ulipotoka kuliko vile wao walivyopotoka katika mienendo yako yote. Kama vile ninavyoishi, –ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe– dada yako Sodoma na wabinti zake, hawakufanya maovu kama yale uliyotenda wewe na wabinti zako. Kosa la dada yako Sodoma, lilikuwa hili: yeye pamoja na wabinti wake walipokuwa na chakula nao walifanikiwa sana, walianza kujivuna, wakaacha kuwasaidia wamasikini na wakosefu. Walijivuna, wakafanya machukizo mbele yangu. Kwa hiyo niliwaangamiza mara tu nilipoyaona hayo. Naye Samaria kwa kweli hakutenda hata nusu ya zambi zako. Wewe umefanya machukizo mengi kuliko wao. Ukilinganisha maovu yako na ya dada zako, maovu yao si kitu! Wewe utaibeba haya yako kabisa! Zambi zako ni mbaya zaidi kuliko za wadada zako, kwa kipimo cha kuwafanya wadada zako na zambi zao, waonekane kama hawana kosa. Basi, upate haya na kufezeheka, maana umewafanya wadada zako waonekane kama hawana kosa. Nitawarudishia Sodoma na Samaria pamoja na wabinti zao hali yao njema ya mbele. Nawe vilevile nitakufanikisha kati yao, kusudi ubebe haya yako na kufezeheka, kwa sababu ya mambo yote uliyotenda, ndipo kwa hali yako hiyo wadada zako watajiona kwamba wao ni afazali. Wadada zako, Sodoma na Samaria, pamoja na wabinti zao watairudilia hali yao ya pale mbele. Hata wewe na wabinti zako mutairudilia hali yenu. Kwa majivuno yako ulimuzarau dada yako Sodoma. Haukufanya hivyo mbele uovu wako haujafichuliwa. Sasa umekuwa kama Sodoma. Umekuwa kitu cha kuchekelewa mbele ya wabinti za Edomu na jirani zake wote, na wabinti za Wafilistini jirani zako ambao walikuchukia. Azabu ya uchafu wa tabia na machukizo yako utaibeba wewe mwenyewe. –Ni ujumbe wa Yawe. Bwana wetu Yawe anasema hivi: Nitakutendea wewe Yerusalema kama unavyostahili. Wewe umekizarau kiapo, ukivunja agano. Lakini mimi nitalikumbuka agano langu nililoagana nawe katika siku za ujana wako. Nitafanya nawe agano la milele. Nawe utakumbuka mienendo yako na kupata haya wakati nitakapokupa wadada zako, mukubwa na mudogo, kama wabinti zako, ingawa si kwa sababu ya agano kati yangu na wewe. Mimi nitafanya agano nawe, nawe utatambua kwamba mimi ni Yawe. Nitakusamehe kila kitu ulichotenda. Nawe utakapokumbuka hayo yote uliyotenda utashangaa na kunyamaza kwa sababu ya haya wala hautasubutu kusema tena. –Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe. Neno la Yawe lilinifikia kusema hivi: Wewe mwanadamu! Tega kitendawili, uwaambie Waisraeli fumbo. Uwaambie kwamba Bwana wetu Yawe anasema hivi: Kulikuwa tai mumoja mukubwa sana aliyekuwa na mabawa makubwa, yenye manyoya marefu mengi yenye rangi za kila aina. Tai yule aliruka mpaka kwenye mulima Lebanoni, akatua juu ya kilele cha muti wa mwerezi; akavunja tawi lake la juu zaidi, akalipeleka katika inchi ya wachuuzi, akaliweka katika muji wao mumoja. Kisha akatwaa kichipukizi cha mumea katika inchi ya Waisraeli, akaupanda katika udongo wenye mboleo ambako kulikuwa maji mengi. Mumea ukakomaa na kuwa muzabibu wa aina ya muti unaotambaa; matawi yake yakaelekea yule tai, na mizizi yake ikaingia chini ndani ya udongo. Muzabibu ukatoa matawi na majani mengi. Lakini kulikuwa tai mwingine mukubwa; alikuwa na mabawa makubwa ya manyoya mengi. Basi, ule muzabibu ulikunja mizizi yake, ukamwelekezea matawi yake, kusudi aumwangilie maji. Muzabibu ulikuwa umepandikizwa penye udongo muzuri na karibu na maji mengi, kusudi upate kutoa matawi na kuzaa matunda uweze kuwa muzabibu muzuri sana! Sasa Bwana wenu Yawe anakuuliza: Muzabibu huo utaweza kustawi? Hawataongoa mizizi yake na kuozesha matunda yake na matawi yake machanga kuyanyausha? Hakutahitajika mutu mwenye nguvu au kundi kubwa kuuongoa kutoka ndani ya udongo. Umepandikizwa, lakini, utastawi? Upepo mukali wa mashariki unapovuma juu yake utanyauka; utakaukia palepale kwenye udongo ulikoota. Kisha neno la Yawe lilinifikia kusema hivi: Sasa uwaulize wale watu waasi kama wanaelewa maana ya mufano huo. Uwaambie kwamba, mufalme wa Babeli alikuja Yerusalema, akamwondoa mufalme na wakubwa wake, akawapeleka Babeli. Kisha akachagua mutu mumoja wa jamaa ya kifalme, akafanya naye mapatano, akamwapisha kiapo cha uaminifu. Aliwaondoa wakubwa wengine katika inchi akawapeleka mbali kusudi utawala huo ukuwe zaifu na ushike agano la mufalme wa Babeli. Lakini yule mufalme mupya alimwasi mufalme wa Babeli kwa kuwatuma wajumbe Misri kuomba farasi na waaskari wengi. Mufalme huyo atashinda? Anayefanya hivyo na kuvunja agano lake ataweza kuepuka azabu? Kama vile ninavyoishi, mufalme huyu atakufia katika inchi ya Babeli, inchi ya mufalme yule aliyemuweka kuwa mufalme, na ambaye amezarau kile kiapo na kuvunja lile agano alilofanya naye. Hakika, Mufalme wa Misri pamoja na jeshi lake kubwa hataweza kumusaidia katika vita wakati Wababeli watakapomuzungushia kikingio na kuta kusudi wapate kuwaua watu wengi. Kwa sababu alikizarau kile kiapo na kuvunja lile agano ambalo aliahidi kwa mukono wake mwenyewe na kufanya mambo yale yote, hakika hataokoka. Kwa hiyo, Bwana wetu Yawe anasema hivi: Kama vile ninavyoishi, nitamwazibu vikali kwa sababu amekizarau kiapo alichoapa kwa jina langu na kuvunja agano langu. Nitatandaza wavu wangu juu yake, naye atanaswa katika mutego wangu; nitamupeleka mpaka Babeli na kumuhukumu kwa sababu ya udanganyifu alioufanya juu yangu. Waaskari wake hodari watauawa kwa upanga na wale watakaoponyoka watatawanyika pande zote. Kwa hiyo mutatambua kwamba ni mimi, kweli ni mimi Yawe ninayesema hivyo. Bwana wetu Yawe anasema hivi: Mimi mwenyewe nitatwaa kichipukizi cha incha ya juu ya muti wa mwerezi. Nitavunja tawi changa kutoka matawi yake ya juu na kulipanda juu ya mulima murefu sana. Kweli, nitalipanda juu ya mulima murefu wa inchi ya Waisraeli kusudi lichanue na kuzaa matunda. Litakuwa mwerezi muzuri, na ndege wa aina zote watakaa chini yake vilevile watajenga chicha zao katika matawi yake. Halafu miti yote katika inchi itajua kwamba mimi Yawe ninaishusha miti mirefu na kuinua miti mifupi. Mimi ninakausha miti mibichi na kustawisha miti yenye kukauka. Ni mimi Yawe ninayesema hayo na nitayafanya. Neno la Yawe lilinifikia kusema hivi: Kwa nini munarudiliarudilia mezali hii katika inchi ya Waisraeli: Wababa wamekula matunda mabichi ya mizabibu, lakini ni meno ya watoto wao ndiyo yanaumizwa! Kama vile ninavyoishi, mezali hii haitatumiwa tena katika Israeli. –Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe.– Mujue kwamba uzima wa kila mutu ni katika mikono yangu, ikiwa uzima wa muzazi na uzima wa mutoto. Yeyote anayetenda zambi, ndiye atakayekufa. Lakini baba yake, kwa sababu alilipisha bei isiyokuwa ya haki na kumwibia ndugu yake, wala hakuwatendea wandugu zake vizuri, hakika atakufa kwa sababu ya uovu wake. Lakini munauliza: Kwa nini mutoto asiazibiwe kwa sababu ya zambi za baba yake? Mutoto akitenda mambo ya haki na ya ukweli, kama akiwa mwangalifu kushika masharti yangu yote, basi, huyo hakika ataishi. Atakayetenda zambi huyo ndiye atakayekufa. Mutoto hatabeba uovu wa baba yake, wala baba hatabeba uovu wa mutoto wake. Uhaki wa mutu wa haki itamufalia yeye mwenyewe: na uovu wa mwovu ataubeba yeye mwenyewe. Kama mutu mwovu akiachana na zambi zake zote alizotenda, kama akishika masharti yangu yote, na kutenda mambo ya haki na ya ukweli, huyo hakika ataishi, hatakufa. Makosa yake yote aliyofanya hayatakumbukwa; kwa sababu ya haki yake ataishi. Basi, ninafurahia kufa kwa mutu mwovu? Hapana! Mimi ninapendelea aachane na njia zake mbaya apate kuishi. –Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe. Lakini, mutu wa haki akiacha haki yake na kutenda uovu na kufanya machukizo yaleyale mutu mwovu anayofanya, basi, huyo ataishi? Hapana! Matendo yake yote mema aliyotenda hayatakumbukwa tena; atakufa kwa sababu ya uasi na zambi aliyotenda. Lakini ninyi munasema: Matendo ya Yawe si sawa! Musikilize sasa, enyi Waisraeli: Ninachofanya mimi si sawa? Munachofanya ninyi ndicho kisichokuwa sawa. Mutu wa haki akiacha haki yake na kutenda uovu atakufa kwa ajili hiyo; atakufa kwa sababu ya uovu aliotenda. Lakini mutu mwovu akiachana na uovu aliofanya, na kutenda mambo ya haki na ya ukweli, huyo atayaokoa maisha yake. Kwa sababu amefikiri, akaachana na makosa aliyoyafanya, hakika ataishi; hatakufa. Lakini ninyi Waisraeli munasema: Anachotenda Yawe si sawa! Enyi Waisraeli, basi, ninachofanya mimi si sawa? Munachofanya ninyi ndicho kisichokuwa sawa. Kwa hiyo, nitawahukumu ninyi Waisraeli, kila mumoja wenu, kulingana na mwenendo wake. –Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe.– Mugeuke na kuachana na makosa yenu yasipate kuwaangamiza. Mutupilie mbali zambi mulizonitendea; mujipatie moyo na roho mupya. Enyi Waisraeli, mutakufa kwa sababu gani? Sifurahii kifo cha mutu yeyote. Hivyo mugeuke kusudi mupate kuishi. –Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe. Mungu aliniambia niimbe wimbo huu wa maombolezo juu ya wakubwa wa Waisraeli: Mama yenu alikuwa simba mwenye utukufu kati ya simba wengine. Alikaa kati ya simba wakali, akawalisha watoto wake. Alimulea mutoto mumoja kati ya watoto wake, mutoto huyo naye akakuwa simba mukali. Akajifunza toka kwa mama yake kuwinda, akakuwa simba mukula watu. Mataifa yakatangaza habari ya hatari juu yake, wakamunasa katika mutego wao, wakamupeleka juu ya ndoana mpaka Misri. Mama yake alipoona kwamba amechoka kungoja, matumaini ya kumupata yakakwisha, akamutwaa mutoto wake mwingine, akamufanya simba mukali. Huyo alipokuwa amekwisha kukomaa, akaanza kutembea pamoja na simba wengine. Naye vilevile akajifunza kuwinda, akakuwa simba mukula watu. Alishambulia nyumba za watu na kuiharibu miji yao. Inchi pamoja na wakaaji wake viliogopa, kwa sauti ya kunguruma kwake. Mataifa yakamushambulia kutoka pande zote, wakatandaza wavu wao juu yake, naye akanaswa katika mutego wao. Kwa ndoana wakamutia katika kizimba chao, wakamupeleka kwa mufalme wa Babeli. Kule, wakamutia katika kifungo, kusudi ngurumo yake isisikilike tena juu ya milima ya Waisraeli. Mama yako alikuwa kama muzabibu katika shamba, uliopandikizwa pembeni ya maji, ambao ulizaa sana kwa kuwa na maji mengi. Ulikuwa na matawi yenye nguvu, ambayo yalikuwa fimbo za kifalme. Muzabibu huo ulikomaa kupita miti mingine, watu walisifu ukubwa wa shina lake na wingi wa matawi yake. Lakini uliongolewa kwa hasira, ukatupwa chini juu ya udongo; upepo mukali wa mashariki ukaukausha, matunda yake yakaanguka; matawi yake yenye nguvu yalikauka, nao moto ukauteketeza. Na sasa umepandikizwa katika jangwa, katika inchi yenye kukauka isiyokuwa na maji. Lakini moto umetoka kwenye shina lake, ukayateketeza matawi na matunda yake. Matawi yake hayatakuwa na nguvu hata kidogo, wala hayatakuwa fimbo za kifalme. Huo umekuwa wimbo wa maombolezo; ndivyo unavyoimbwa siku zote. Mwaka wa saba tangu kuhamishwa kwetu, siku ya kumi ya mwezi wa tano, wazee wamoja wa Waisraeli walikuja kumwuliza Yawe shauri, wakaikaa mbele yangu. Basi, neno la Yawe lilinifikia kusema hivi: Wewe mwanadamu, sema na hao wazee wa Waisraeli. Uwaambie kwamba: Bwana wetu Yawe anasema hivi: Mumekuja kuniuliza shauri? Kama vile ninavyoishi, sitakubali kuulizwa shauri na ninyi. –Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe.– Wewe mwanadamu, uko tayari kuwahukumu watu hawa? Basi, uwahukumu. Uwajulishe mambo wazee wao waliyofanya. Uwaambie kwamba Bwana wetu Yawe anasema hivi: Siku ile nilipowachagua Waisraeli niliwaapia wazao wa Yakobo. Nilijijulisha kwao katika inchi ya Misri, nikawaapia nikisema: Mimi ni Yawe, Mungu wenu. Siku hiyo niliwaapia kwamba nitawatoa katika inchi ya Misri na kuwapeleka mpaka kwenye inchi niliyowachagulia, inchi ya maziwa na asali na inchi nzuri kuliko inchi zote. Niliwaambia: Mutupilie mbali machukizo yote munayoyapenda; musijichafue na sanamu za miungu ya Misri, kwa maana mimi ni Yawe, Mungu wenu. Lakini waliniasi, hawakutaka kunisikiliza. Hakuna hata mumoja kati yao aliyetupilia mbali machukizo yale waliyoyapenda, wala hawakuachana na sanamu za miungu ya Misri. Basi, nikafikiri kwamba nitawamwangia kasirani yangu na kuitimiza hasira yangu juu yao wakiwa kulekule katika inchi ya Misri. Lakini nilijizuiza kufanya hivyo kwa heshima ya jina langu kusudi lisizarauliwe kati ya watu wa mataifa wanaoishi nao, hao walioona nikijijulisha kwa Waisraeli wakati wa kuwatoa katika inchi ya Misri. Basi, mimi niliwatoa katika inchi ya Misri, nikawapeleka katika jangwa. Niliwapa masharti yangu na kuwafundisha maagizo yangu ambayo mutu akiyafuata ataishi. Niliwapa vilevile Sabato zangu zikuwe kitambulisho kati yangu na wao, wapate kujua kwamba mimi ni Yawe ninayewatakasa. Lakini Waisraeli waliniasi kule katika jangwa; hawakuyafuata masharti yangu, lakini walikataa maagizo yangu ambayo mutu akiyafuata ataishi. Sabato zangu walizikufuru siku zote, nami nikasema kwamba nitawamwangia kasirani yangu na kuwaangamiza kulekule katika jangwa. Lakini nilijizuiza kufanya hivyo kwa heshima ya jina langu kusudi lisizarauliwe kati ya watu wa mataifa ambao waliona jinsi nilivyowatoa Waisraeli katika inchi ya Misri. Hata hivyo, niliwaapia kulekule katika jangwa kwamba sitawaingiza katika inchi niliyowapa, inchi ya maziwa na asali na inchi nzuri kuliko inchi zote. Nilifanya hivyo kwa sababu waliyakataa maagizo yangu, hawakufuata masharti yangu, wakazikufuru Sabato zangu; maana walijitoa kwa moyo juu ya sanamu za miungu yao. Lakini nikawaonea huruma, sikuwaangamiza kule katika jangwa. Niliwaonya wazao wao kule katika jangwa: Musifuate masharti ya wazee wenu, musishike maagizo yao wala musijichafue kwa kuziabudu sanamu za miungu yao. Mimi Yawe ni Mungu wenu. Mufuate masharti yangu, mushike maagizo yangu kwa uangalifu. Mufanye Sabato zangu kuwa takatifu, kusudi zikuwe kitambulisho cha agano langu nanyi. Hizo zitawakumbusha kwamba mimi Yawe ni Mungu wenu. Lakini hata wazao wao hao waliniasi. Hawakufuata masharti yangu, hawakushika wala kutimiza maagizo yangu ambayo mutu akiyashika, ataishi. Walizikufuru Sabato zangu. Basi nikasema kwamba nitawamwangia kasirani yangu na kuitimiza hasira yangu juu yao kule katika jangwa. Lakini nilizuiza mukono wangu kwa sababu ya heshima ya jina langu kusudi nisizarauliwe kati ya watu wa mataifa walioona nikiwatoa katika inchi ya Misri. Hata hivyo, niliapa kulekule katika jangwa kwamba ningewapeleka katika inchi za mbali na kuwafanya waishi kati ya mataifa ya kigeni, kwa sababu hawakufuata maagizo yangu, lakini waliyakataa masharti yangu, wakazikufuru Sabato zangu na kuziabudu sanamu za miungu ya wazee wao. Tena niliwapa masharti mabaya na maagizo ambayo hayawezi kuwawezesha kuishi. Nikawaacha wajichafue kwa sadaka zao za kuwatoa wazaliwa wao wa kwanza sadaka ya kuteketezwa kwa moto. Hili lilikuwa pigo lao la azabu ya kutisha kusudi watambue kwamba mimi ni Yawe. Sasa, wewe mwanadamu, uwaambie Waisraeli kwamba: Bwana wetu Yawe anasema hivi: Wazee wenu walinikufuru kila mara kwa kukosa uaminifu. Maana nilipowapeleka katika ile inchi niliyoapa kuwapa, kila mara walipoona kilima kirefu au miti ya majani mengi, walianza kutoa matambiko na sadaka zao na kunichokoza. Kulekule walitoa sadaka za harufu nzuri na kutoa sadaka za kinywaji. (Mimi nikawauliza: Pahali hapo palipoinuka munapokwenda panaitwa namna gani? Wao wakapaita Pahali Palipoinuka mpaka leo.) Basi, uwaambie Waisraeli kwamba: Bwana wetu Yawe anasema hivi: Mutajichafua kwa kufuata desturi za wazee wenu na kuviabudu vitu vinavyonichukiza? Munapoendelea kutoa sadaka zenu na kuwateketeza watoto wenu kwa moto munajichafua mpaka leo hii. Nitaulizwa shauri nanyi, enyi watu wa Israeli? Kama vile ninavyoishi, –ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe– sitakubali kuulizwa shauri nanyi. Ninyi munasema ndani ya mioyo yenu: Tutakuwa kama mataifa mengine, kama makabila ya inchi ingine na kuabudu miti na mawe. Hayo munayofikiri ndani ya mioyo yenu hayatafanikiwa hata kidogo. Kama vile ninavyoishi, –ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe– nitawatawala kwa mukono wenye nguvu, kwa ukali na kuwamwangia kasirani yangu. Nitawatoa kutoka mataifa na kuwakusanya kutoka katika inchi mulimosambazwa kwa mukono wangu wenye nguvu, kwa ukali na kwa kasirani yangu. Nitawapeleka kwenye jangwa la mataifa; na huko nitawahukumu moja kwa moja. Kama nilivyowahukumu wazee wenu kule katika jangwa katika inchi ya Misri, ndivyo nitakavyowahukumu ninyi. –Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe. Nitawalazimisha mukuwe chini ya uchungaji wangu kila mumoja, na kuwaongoza mupate kutii agano langu. Nitaondoa kati yenu waasi na wale wanaonikosea; nitawaondoa katika inchi walikokaa kama wakimbizi, lakini hawataingia hata kidogo katika inchi ya Waisraeli. Halafu mutatambua kwamba mimi ni Yawe. Na sasa, enyi Waisraeli, Bwana wenu Yawe anawaambia hivi: Muendelee kuziabudu sanamu zenu za miungu, kama hamunisikilizi; lakini mutalazimishwa kuacha kulikufuru jina langu takatifu kwa sadaka na sanamu zenu. Maana, katika mulima wangu mutakatifu, mulima murefu wa Israeli, ninyi wote watu wa Israeli mutanitumikia kule. –Ni ujumbe wa Yawe.– Huko mimi nitawapokea na kungojea muniletee sadaka na matoleo yenu bora na matoleo iliyotakaswa. Kisha kuwatoa toka katika inchi ambako mumesambazwa na kuwakusanya pamoja, nitazipokea sadaka zenu zenye harufu nzuri. Nami nitaonyesha utakatifu wangu kati yenu mbele ya mataifa mengine. Nanyi mutatambua kwamba mimi ni Yawe, wakati nitakapowarudisha mpaka katika inchi ya Israeli, inchi niliyoapa kuwapatia wazee wenu. Huko ndiko mutakapokumbuka mwenendo wenu na matendo yenu mabaya ambayo yaliwachafua; nanyi mutachukizwa kabisa kwa sababu ya maovu yote muliyotenda. Halafu mutatambua kwamba mimi ni Yawe, wakati nitakapowatendea ninyi sio kulingana na mwenendo wenu na matendo yenu mabaya, lakini kwa heshima ya jina langu. –Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe. Neno la Yawe lilinifikia kusema hivi: Wewe mwanadamu, geukia upande wa kusini, uhubiri juu ya inchi ya kusini, juu ya wakaaji wa pori la Negebu. Uwaambie wasikilize neno la Yawe. Uwaambie kwamba Bwana wao Yawe anasema hivi: Nitawasha moto kwako, nao utateketeza miti yote, mibichi na yenye kukauka; utaenea tangu kusini mpaka kaskazini wala hakuna atakayeweza kuzimisha ndimi zake. Nao utaunguza watu wote. Watu wote watajua kwamba ni mimi Yawe niliyeuwasha na hautazimika. Kisha nami nikasema: Ee Bwana wetu Yawe! Watu wanalalamika juu yangu na kusema: Huyu akisema, ni mafumbo tu! Neno la Yawe lilinifikia kusema hivi: Wewe mwanadamu, ugeukie upande wa Yerusalema, uhubiri juu ya nafasi zake za kutambikia, na kutoa unabii juu ya inchi ya Waisraeli. Uwaambie Waisraeli kwamba: Yawe anasema hivi: Mimi mwenyewe ninakuja kupambana nanyi. Nitauchomoa upanga wangu ndani ya mufuko wake na kuwaua watu wema na wabaya. Tangia kaskazini mpaka kusini, nitawaua watu wote, wema na wabaya, kwa upanga wangu. Watu wote watajua kwamba mimi Yawe ndiye niliyeuchomoa upanga ndani ya mufuko wake na wala hautarudishwa tena ndani. Nawe mwanadamu, ujikunje kama mutu aliyekata tamaa, uomboleze mbele yao. Wakikuuliza hivi: Kwa nini unaomboleza? Utawaambia: Ninaomboleza kwa sababu ya habari zinazokuja. Kila mutu atavunjika moyo, mikono yao yote itaregea; kila mutu anayeishi atazimia na magoti yao yataregea. Habari hizo zinakuja kweli, nazo zinatimia. –Ni Bwana wetu Yawe anayesema hivyo. Neno la Yawe lilinifikia kusema hivi: Wewe mwanadamu, toa unabii useme: Yawe anasema hivi: Upanga! Kweli, upanga umenolewa, nao umeangarishwa vilevile. Umenolewa kusudi ufanye mauaji, umeangarishwa umetemete kama umeme! Umenolewa na kuangarishwa uwekwe katika mukono wa mwuaji. Wewe mwanadamu, ulie na kuomboleza upanga huo umenyooshwa juu ya watu wangu, juu ya wakubwa wote wa Waisraeli. Wataangamizwa kwa upanga pamoja na watu wangu. Ujipigepige kifua kwa huzuni. Hilo litakuwa jaribu gumu sana. –Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe.– Wewe mwanadamu, utabiri! Piga mikono, upanga ufanye kazi yake, mara mbili, mara tatu. Huo ni upanga wa mauaji nao unawazunguka. Kwa hiyo wamevunjika moyo na wengi wanaanguka. Nimeiweka chongo ya upanga katika milango yao yote. Umefanywa uangae kama umeme, umengarishwa kwa ajili ya mauaji. Ewe upanga, shambulia upande wa kuume, shambulia upande wa kushoto; elekeza chongo yako pande zote. Nami nitapiga mikono, kasirani yangu itatosheka. Ni mimi Yawe ninayesema hivyo. Neno la Yawe lilinifikia kusema hivi: Wewe mwanadamu! Chora njia mbili ambapo upanga wa mufalme wa Babeli utapitia. Njia zote mbili zianzie katika inchi moja. Kwa mwanzo wa kila njia utaweka kitambulisho cha kuonyesha upande muji unapokuwa. Utachora njia upanga utakapopitia kwenda kuufikilia muji Raba wa Waamoni, na njia ingine inayoelekea Yerusalema wenye kuzungukwa na kuta katika inchi ya Yuda. Mufalme wa Babeli anasimama kwa mwanzo wa hizo njia mbili, kwenye masanganjia, apate kuaguza. Anatikisa mishale, anauliza shauri la sanamu ya miungu yake na kuchunguza maini ya nyama. Mushale ulioangukia kwa upande wa mukono wake wa kuume, ulionyesha Yerusalema. Pale wataweka vifaa vya vita kwa kuubomoa. Anaamuru mauaji, kelele za vita zipigwe, vifaa vya vita kwa kubomoa milango viwekwe, lundo ya udongo na minara kwa kuushambulia muji viwekwe vilevile. Lakini watu wa Yerusalema watauzania kuwa ni utabiri wa uongo kwa sababu ya mapatano waliyofanya. Hata hivyo unabii huu utawakumbusha uovu wao na kusababisha kukamatwa kwao. Kwa hiyo, Bwana wetu Yawe anasema hivi: Wote wataweza kuziona zambi zenu. Kila mutu atajua jinsi munavyokuwa na makosa. Kila kitendo munachotenda kinaonyesha zambi zenu. Ninyi mutapata azabu nami nitawatia katika mikono ya waadui zenu. Nawe, mufalme wa Waisraeli, wewe ni mupotovu kabisa. Siku yako imefika, siku ya azabu yako ya mwisho. Bwana wetu Yawe anasema hivi: tosha kitambulisho chako cha kifalme na taji yako, maana mambo hayatabaki kama yalivyokuwa. Wanaokuwa chini watanyanyuliwa, wanaokuwa juu watashushwa! Uharibifu! Uharibifu! Hakuna chochote katika muji huu nitakachoacha. Lakini mbele ya hayo kutafika kwanza yule ambaye nimemupa mamlaka ya kuuazibu, ambaye mimi nitamupa muji ule. Ewe mwanadamu, tabiri juu ya Waamoni na maneno yao ya kuwachekelea Waisraeli: Uwaambie kwamba ninasema hivi: Upanga, upanga! Upanga umenyooshwa kwa kuua, umenolewa upate kuangamiza, umengarishwa uangae kama umeme. Wakati ninyi mumetulia katika maono yenu madanganyifu na utabiri wenu wa uongo, upanga utakuwa tayari kukata shingo za waasi na waovu. Siku imetimia ambapo maovu yenu yataazibiwa. Sasa rudisha upanga ndani ya mufuko wake! Nitawahukumu pahali palepale mulipoumbwa, katika inchi mulipozaliwa. Nitawamwangia kasirani yangu. Moto wa kasirani yangu nitaupuliza juu yenu. Nitawatoa katika mikono ya watu waovu, watu hodari wa kuangamiza. Mutakuwa kama kuni ndani ya moto, damu yenu itamwangika katika inchi. Mutu hatawakumbuka tena. Ni mimi Yawe ninayesema hivyo. Neno la Yawe lilinifikia kusema hivi: Ewe mwanadamu! Uko tayari kutoa hukumu, kuuhukumu muji huu wa wauaji? Basi, ujulishe machukizo yake yote. Uuambie kwamba: Bwana wetu Yawe anasema hivi: Wewe ni muji unaowaua watu wako mwenyewe na kujichafua kwa kufanya sanamu za miungu; kwa hiyo wakati wako wa azabu umetimia. Una makosa kutokana na damu uliyomwanga. Umejichafua kwa sanamu ulizojifanyia. Umeileta siku yako ya azabu karibu nawe; siku zako zimehesabiwa. Ndiyo maana nimekufanya uchekelewe na mataifa na kuzarauliwa na inchi zote. Inchi zote za mbali na za karibu zitakuchekelea. Umejipatia sifa mbaya na kujaa fujo. Wakubwa wa Waisraeli wanaokuwa humo, kila mumoja kadiri ya nguvu zake anaua watu. Kwako baba na mama wanazarauliwa. Mugeni anayekaa kwako ananyanganywa mali yake. Wayatima na wajane wanaonewa. Wewe umezarau vyombo vyangu vitakatifu na kuzikufuru Sabato zangu. Kwako kuna wanaowasingizia wengine kusudi wauawe. Wakaaji wako wanashiriki chakula kilichotolewa kwa miungu juu ya milima. Watu wako wanatenda uasherati. Kwako kuna watu ambao wanalala na wake wa baba zao. Wanalala kwa kinguvu na wanawake katika siku zao za ugonjwa wa mwezi. Wengine wanafanya machukizo kwa kulala na wake za jirani zao. Wengine wanalala na wake za watoto wao, na wengine wanalala na wadada zao. Huko kwako kuna watu ambao wanapokea kitulizo kwa kumwanga damu. Wanakopesha kwa kudai faida ya juu, wananyanganya mali za wenzao kwa nguvu, na kunisahau mimi kabisa! –Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe.– Nimekunja ngumi yangu juu yako kwa sababu ya hiyo faida uliyopata kwa njia isiyokuwa ya haki na kwa mauaji yaliyofanyika kwako. Utaweza kuvumilia kuwa hodari siku nitakapokushambulia? Ni mimi Yawe ninayesema hivyo na nitakayetimiza hayo. Nitakusambaza kati ya mataifa na kukutupatupa katika inchi zingine. Nitaukomesha uchafu unaokuwa ndani yako. Utajichafua mbele ya mataifa mengine, lakini utatambua kwamba mimi ni Yawe. Tena neno la Yawe lilinifikia kusema hivi: Wewe mwanadamu! Waisraeli wamekuwa kwangu kama takataka. Wao ni kama takataka inayobaki wakati madini ya shaba, bati, chuma au risasi yanaposafishwa. Kwa hiyo, Bwana wetu Yawe anasema hivi: Kwa kuwa ninyi wote mumekuwa takataka ya madini, mimi nitawakusanya pamoja katika Yerusalema. Kama vile watu wanavyokusanya feza, shaba, chuma, risasi na bati katika furu wapate kuzisafisha kwa moto, ndivyo kasirani na hasira yangu vitakavyowakusanya huko na kuwayeyusha. Nitawakusanya na kuwawasha moto kwa kasirani yangu; nanyi mutayeyuka mukiwa humo ndani ya muji. Kama feza inavyoyeyuka katika furu, ndivyo mutakavyoyeyushwa humo katika muji. Nanyi mutatambua kwamba mimi Yawe nimeimwanga kasirani yangu juu yenu. Neno la Yawe lilinifikia kusema hivi: Wewe mwanadamu! Uwaambie Waisraeli kwamba inchi yao ni kama inchi ambayo haijanyeshewa, imenyauka kwa sababu ya kasirani yangu ikakuwa kama udongo bila maji. Wakubwa wenu ni kama simba anayenguruma anaporarua nyama wake. Wanaua watu, wanawanyanganya watu mali na vitu vyao vya bei kali, na kuongeza hesabu ya wajane. Makuhani wao wanavunja sheria zangu, na kukufuru vyombo vyangu vitakatifu. Hawapambanui kati ya vitu vitakatifu na vitu visivyokuwa vitakatifu, wala hawafundishi watu tofauti kati ya mambo yanayokuwa machafu na yanayokuwa safi. Wameacha kuzishika Sabato zangu, na kunizaraulisha kati yao. Wakubwa wake wanaokuwa ndani ya muji ni kama imbwa wa pori wanaorarua nyama wao; wanaua kwa kujitajirisha kwa namna isiyokuwa ya haki. Manabii wake wanaficha maovu hayo kama mutu anapotia chokaa kwenye ukuta wenye kuharibika. Wanapata maono ya uongo na kutabiri udanganyifu mutupu, wakisema “Bwana wetu Yawe anasema hivi”, wakati mimi mwenyewe sikuwaambia chochote. Kila fasi katika inchi watu wanatendeana vibaya na kunyanganya kwa kinguvu. Wanagandamiza wamasikini na wakosefu, na kuwaonea wageni bila kujali. Nilitafuta kati yao mutu mumoja atengeneze ukuta na kusimama juu ya nafasi iliyobomoka mbele yangu, kusudi ailinde inchi na kunizuia nisiiharibu, lakini sikumupata hata mumoja. Kwa hiyo nimewamwangia kasirani yangu na kwa moto wa hasira yangu nimewateketeza kulingana na matendo yao. –Ndivyo anavyosema Bwana wetu Yawe. Neno la Yawe lilinifikia kusema hivi: Wewe mwanadamu! Kulikuwa wabinti wawili, wote wa mama mumoja. Katika ujana wao walipokuwa wanakaa kule Misri, wakakubali maziba yao kupapaswa, wakapoteza ubikira wao, wakafanya uzinzi. Yule mukubwa aliitwa Ohola, na yule mudogo Oholiba. Basi, wote wakakuwa wangu, wakanizalia watoto, wana na wabinti. Basi, Ohola ni Samaria na Oholiba ni Yerusalema! Ingawa Ohola alikuwa muke wangu, lakini aliendelea kuwa muzinzi na kuwatamani wapenzi wake Waasuria. Kati yao kulikuwa waaskari, wenye kuvaa nguo za bei kali za rangi nyekundu-nyeusi, kulikuwa vilevile maliwali na waamuzi. Wote walikuwa vijana wa kuvutia na waaskari wapanda-farasi hodari. Ohola alifanya uasherati na wale wakubwa wote wenye vyeo vya juu wa Waasuria, naye akajichafua kwa kuabudu sanamu zote kila mwanaume wake aliyetamani. Aliendelea na uzinzi wake aliouanza kule Misri wakati huo wa ujana wake, wanaume walivunja ubikira wake na kuzitimiza tamaa zao kwake. Kwa hiyo nikamutoa katika mikono ya Waasuria wapenzi wake, ambao aliwatamani sana. Hao walimuvua nguo zake na kumwacha uchi. Waliwakamata watoto wake, naye mwenyewe wakamwua kwa upanga. Azabu hiyo aliyopata ikakuwa fundisho kwa wanawake wengine. Dada yake Oholiba aliona jambo hilo, lakini akazidi kupotoka kuliko yeye katika tamaa yake, na uzinzi wake ulikuwa mubaya kuliko wa dada yake. Aliwatamani sana Waasuria: maliwali, waamuzi, waaskari waliovaa nguo zao za kiaskari, waaskari wapanda-farasi hodari, wote wakiwa vijana wa kuvutia. Nilimutambua kuwa muchafu. Kweli wote wawili walikuwa na tabia hiyo moja. Lakini Oholiba alizidisha uzinzi wake; akapendezwa na picha za Wakaldea za rangi nyekundu zilizochorwa juu ya ukuta, na mikaba katika viuno, vitambaa vikubwa juu ya vichwa; hizo zote zilifanana na wakubwa. Ni picha ya Wababeli, wakaaji wa inchi ya Kaldea. Alipoziona picha hizo, mara moja akashikwa na tamaa, akatuma wajumbe kwenda Kaldea. Basi, Wababeli wakamwendea katika kitanda cha mapenzi. Wakamuchafua kwa njia ya tamaa zao mbaya. Alipokwisha kujichafua, akajitenga nao. Alipoendelea na uzinzi wake na kufunua uchi wake, mimi nilimwacha kama nilivyomwacha dada yake. Hata hivyo, akazidisha uzinzi wake akifanya kama wakati wa ujana wake alipofanya uzinzi kule Misri. Aliwatamani sana wanaume wenye viungo kama viungo vya punda na wenye kuwaka tamaa kama farasi dume. Oholiba aliutamani uchafu wake wa ujana alipokuwa Misri, ambako Wamisri walivunja ubikira wake, na kuyapapasa maziba yake machanga. Sasa Oholiba, Bwana wetu Yawe anasema hivi: Nitawasukuma wapenzi wako, wale uliochukizwa nao wakushambulie; nitawaleta wakushambulie kutoka pande zote. Nitawachochea Wababeli na Wakaldea wote, watu toka Pekodi, Soa na Koa, pamoja na Waasuria wote. Nitawachochea vijana wote wa kuvutia, maliwali, waamuzi, majemadari na waaskari wote wakiwa wapanda-farasi. Watakuja kutoka upande wa kaskazini, pamoja na magari ya vita na ya mizigo, wakiongoza kundi kubwa la watu. Watakuzunguka pande zote kwa ngao kubwa na ndogo na kofia za chuma. Nimewapa uwezo wa kukuhukumu, nao watakuhukumu kadiri ya sheria zao. Nami nitakuelekezea kasirani yangu, nao watakutendea kwa hasira kali. Watakukata pua na masikio na watu wako watakaobaki watauawa kwa upanga. Watawatwaa wana na wabinti zako, na watu wako watakaobaki watateketezwa kwa moto. Watakuvua nguo zako na kukunyanganya vitu vyako vizuri vya bei kali. Nitaukomesha uasherati na uzinzi wako ulioufanya tangu ulipokuwa kule Misri. Hautaziangalia sanamu zozote tena wala kuifikiria tena inchi ya Misri. Kweli, Bwana wetu Yawe anasema hivi: Nitakutia katika mikono ya watu unaowachukia, watu unaowaona kuwa kinyaa. Kwa vile wanakuchukia, watakunyanganya matunda yote ya kazi yako na kukuacha uchi, bila nguo na kuonyesha haya ya uzinzi wako. Uzinzi wako na uasherati wako ndivyo vilivyokuletea hali hiyo. Wewe ulizini na mataifa, ukajichafua kwa kuabudu miungu yao. Kwa sababu ulifuata njia ya dada yako, basi, mimi nitakupa kikombe kilekile cha azabu ukikunywe. Bwana wetu Yawe anasema hivi: Utakunywa toka kikombe cha dada yako; kikombe kikubwa na kirefu. Watu watakuchekelea na kukuzarau; na kikombe chenyewe kimejaa. Kitakulewesha na kukuhuzunikisha sana. Kikombe cha dada yako Samaria, ni kikombe cha hofu na maangamizi. Utakikunywa na kukimaliza kabisa; utakipasua vipandevipande kwa meno, na kurarua navyo maziba yako. –Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe. Kwa hiyo Bwana wetu Yawe anasema hivi: Kwa kuwa umenisahau na kunigeuzia mugongo, basi, utabeba muzigo wa uasherati na uzinzi wako. Yawe aliniambia: Wewe mwanadamu! Uko tayari kuwahukumu Ohola na Oholiba? Basi, uwatangazie matendo yao ya kuchukiza! Wamefanya uzinzi na mauaji. Wamefanya ukahaba kwa sanamu zao, hata kuzitambikia watoto walionizalia wao wenyewe. Tena si hayo tu! Wamekufuru hekalu langu na kuvunja Sabato zangu. Siku ileile walipozitambikia watoto wao wenyewe kwa sanamu, waliingia Pahali Patakatifu pangu kusudi wapachafue. Hayo ndiyo waliyofanya katika nyumba yangu. Hata walituma wajumbe wawaite watu wa mbali, nao wakakuja. Kwa ajili yao, walikoga, wakajitia wanja na kuvaa vitu vya kujipamba. Kisha wakaikaa kwenye vitanda vizurivizuri, na mbele yao meza imetandikwa. Juu ya meza hiyo uliweka ubani wangu na mafuta yangu. Basi, kukasikilika sauti za kundi la watu wasiojali kitu, kundi la wanaume walevi walioletwa kutoka katika jangwa. Waliwavalisha hao wanawake vikomo kwa mikono yao na taji nzuri juu ya vichwa vyao. Halafu nikasema: Wanazini na mwanamuke aliyechakaa kwa uzinzi. Kila mumoja alimwendea kama wanaume wanavyomwendea kahaba. Ndivyo walivyowaendea Ohola na Oholiba wale wanawake waasherati. Lakini waamuzi wa haki watawahukumu jinsi wanavyohukumu wazinzi na wauaji; kwa maana ni wazinzi na wauaji. Basi, Bwana wetu Yawe anasema hivi: Kundi la watu litaletwa, litawatisha na kuwanyanganya mali zao. Kundi hilo la watu litawapiga mawe, litawashambulia kwa upanga na kuwaua wana wao na wabinti zao, na nyumba zao wataziteketeza kwa moto. Ndivyo nitakavyokomesha uasherati wao katika inchi nzima, ikuwe onyo kwa wanawake wote wasifanye uzinzi kama huo mulioufanya. Na ninyi Ohola na Oholiba, mutaazibiwa kutokana na uzinzi wenu na zambi yenu ya kuziabudu sanamu za miungu. Halafu mutatambua kwamba mimi ni Bwana wenu Yawe. Katika siku kumi, ya mwezi wa kumi, kwa mwaka wa kenda tangu kuhamishwa kwetu, neno la Yawe lilinifikia kusema hivi: Wewe mwanadamu! Andika tarehe ya siku ya leo, maana hii ni siku ambapo mufalme wa Babeli anaanza kuushambulia Yerusalema. Uwape mufano hao watu wangu waasi na kuwaambia kwamba: Bwana wetu Yawe anasema hivi: Weka chungu juu ya mafika, ukijaze maji vilevile. Tia humo vipande vya nyama, vipande vizuri vya paja na mabega. Ukijaze vilevile mifupa mizuri. Tumia nyama nzuri ya kondoo, panga kuni chini ya chungu, tokotesha vipande vya nyama na mifupa, vyote uvitokoteshe vizuri. Basi, Bwana wetu Yawe anasema hivi: Ole kwake muji wa mauaji! Muji huo ni kama chungu chenye kutu, ambacho kutu yake haiwezi kutoka! Vipande vya nyama ndani yake vinatoshwa kimoja kimoja bila kuchaguliwa. Mauaji yako humo katika muji; damu yenyewe haikumwangwa juu ya udongo kusudi ifunikwe na mavumbi, lakini ilimwangwa juu ya jiwe. Damu hiyo nimeiacha huko juu ya jiwe kusudi isifunikwe, nipate kuamusha kasirani yangu na kulipiza kisasi. Kwa hiyo, Bwana wetu Yawe anasema hivi: Ole kwake muji wa mauaji! Mimi nitalundika lundo kubwa la kuni. Kusanya vipande vya kuni na kuwasha moto. Tokotesha nyama vizuri sana. Tokotesha na kukausha muchuzi, na mifupa ipate kuungua! Weka chungu kitupu juu ya makaa kipate moto sana, shaba yake ipate moto, uchafu wake uyeyushwe na kutu iunguzwe. Lakini ni kujisumbua bure; kutu yake nene haitoki hata kwa moto. Ewe Yerusalema, matendo yako machafu yamekuchafua. Ingawa nilijaribu kukutakasa, mwenyewe ulibaki muchafu. Basi, hautatakasika tena mpaka nitakapotuliza hasira yangu juu yako. Ni mimi Yawe ninayesema hivyo. Jambo hilo litakamilika; mimi nitalitenda. Sitajuta jambo hilo wala kukuonea huruma. Nitakuazibu kulingana na mwenendo na matendo yako. –Ni Bwana wetu Yawe anayesema hivyo. Neno la Yawe lilinifikia kusema hivi: Wewe mwanadamu! Kwa rafla nitakuondolea mupenzi wako. Lakini usiomboleze, wala kulia, wala kutoa machozi. Utaugua, lakini sio kwa sauti. Hautamufanyia kilio huyo aliyekufa. Vaa viatu vyako na kuvaa kitambaa; usiufunike uso wako wala kula chakula cha kilio. Basi, asubui nilisema na watu, na magaribi muke wangu akakufa. Na kesho yake asubui, nilifanya kama nilivyoamuriwa. Watu wakaniuliza hivi: Jambo hili unalofanya lina maana gani? Nikawajibu: Neno la Yawe lilinifikia kusema hivi: Uwaambie Waisraeli kwamba: Bwana wetu Yawe anasema hivi: Nitalichafua hekalu langu, hiyo nyumba ambayo munajivunia na kuitegemea na ambao munafurahi sana kuiona. Ninyi mutafanya kama vile Ezekieli alivyofanya. Hamutazifunika nyuso zenu wala kula chakula cha kilio. Mutavaa vitambaa kwa kichwa na viatu; hamutaomboleza, wala kulia. Kutokana na maovu yenu, mutaregea na kuugua, kila mutu na mwenzake. Naye Ezekieli atakuwa kitambulisho kwenu: mutafanya kila kitu kama vile alivyotenda. Wakati mambo hayo yatakapotukia, mutatambua kwamba mimi ni Bwana wenu Yawe. Yawe akaniambia hivi: Wewe mwanadamu! Siku ile nitakapoondoa kwao hicho ambacho ni tegemeo lao, na sababu ya shangwe yao, pahali ambapo wanapenda sana kupaona, nitawaondoa wana wao na wabinti zao. Siku hiyo, mutu atakayeponyoka atakuja kukupasha habari hizo. Siku hiyohiyo, utaacha kuwa bubu, nawe utaweza kuongea naye. Kwa hiyo wewe utakuwa kitambulisho kwao, nao watatambua kwamba mimi ni Yawe. Neno la Yawe lilinifikia kusema hivi: Wewe mwanadamu! Ugeukie upande wa inchi ya Waamoni, utoe unabii juu yao. Uwaambie Waamoni hivi: Musikilize neno la Bwana wetu Yawe: Ninyi mulifurahia kuona hekalu langu likichafuliwa, inchi ya Waisraeli ikiangamizwa na watu wa Yuda wakipelekwa katika uhamisho. Basi, nitawatoa ninyi katika mikono ya watu wa mashariki; watapiga hema zao kati yenu na kufanya makao yao katika inchi yenu. Nao watakula matunda yenu na kunywa maziwa yenu. Nitaufanya muji wa Raba kuwa nafasi ya kukulishia ngamia na inchi ya Amoni kuwa zizi la kondoo. Halafu mutatambua kwamba mimi ni Yawe. Bwana wetu Yawe anasema hivi: Kwa sababu mulipiga mikono, mukarukaruka kwa furaha na kushangilia sana juu ya inchi ya Waisraeli, basi, mimi nimeunyoosha mukono juu yenu kwa kuwaazibu; nitawaacha mukamatwe mateka na watu wa mataifa mengine. Nitawaangamiza kabisa, nanyi hamutakuwa taifa tena wala kuwa na inchi. Kwa hiyo mutatambua kwamba mimi ni Yawe. Bwana wetu Yawe alisema: Kwa sababu Wamoabu wamesema kwamba watu wa inchi ya Yuda ni sawa tu na mataifa mengine, mimi nitaifanya miji inayolinda mipaka ya Moabu ishambuliwe, hata miji ile bora kabisa, ni kusema Beti-Yesimoti, Bali-Meoni na Kiriataimu. Nitatoa inchi hiyo pamoja na inchi ya Waamoni katika mikono ya watu wa mashariki wakuwe mali yao. Inchi ya Moabu haitakuwa taifa tena. Mimi nitaiazibu inchi ya Moabu, nao watatambua kwamba mimi ni Yawe. Bwana wetu Yawe alisema hivi: Kwa sababu Waedomu wamefanya kisasi na Yuda, wakawalipiza watu wa Yuda kisasi kibaya sana basi, Bwana wetu Yawe anasema: Nitanyoosha mukono juu ya inchi ya Edomu kwa kuwaazibu na kuwaua watu wote na nyama. Nitaifanya kuwa ukiwa kutoka muji wa Temani mpaka muji wa Dedani. Watu wa inchi hiyo watauawa kwa upanga. Nitawafanya watu wangu Waisraeli walipize kisasi juu ya Waedomu nao watawatendea Waedomu kadiri ya hasira na kasirani yangu. Halafu Waedomu watatambua uzito wa kisasi changu. –Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe. Bwana wetu Yawe anasema hivi: Kwa sababu Wafilistini walifanya kisasi, wakawalipiza kisasi waadui zao kwa ubaya sana na kuendelea kuwa waadui zao siku zote, basi, mimi Bwana wenu Yawe ninawaambia hivi: Nitanyoosha mukono juu ya Wafilistini kwa kuwaazibu; nitawaangamiza hao watu wa Kereti na wakaaji wa kandokando ya bahari. Nitawalipiza kisasi kikali kwa azabu ya kasirani. Halafu watatambua kwamba mimi ni Yawe. Katika siku ya kwanza ya mwezi, mwaka wa kumi na mumoja tangia kuhamishwa kwetu, neno la Yawe lilinifikia kusema hivi: Wewe mwanadamu! Watu wa muji wa Tiro wameuchekelea Yerusalema na kusema: Aha! Yerusalema muji ambao watu wote walipitia, umeangamizwa! Sasa umetuachia nafasi; utajiri wake umeharibika! Basi, Bwana wetu Yawe anasema hivi: Sasa nitapingana nawe ewe Tiro. Nitasukuma mataifa mengi juu yako, nao watakuja kama mawimbi ya bahari. Wataziharibu kuta zako na kuibomoa minara yako. Nitafagia kabisa udongo wako na kukufanya kuwa kama jiwe tupu. Utakuwa pahali penye kukauka katikati ya bahari, na wavuvi watakaushia nyavu zao hapo. –Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe.– Mataifa yatakukamata mateka, na miji inayokuwa jirani yako huko katika vijiji itaangamizwa. Nao watatambua kwamba mimi ni Yawe. Bwana wetu Yawe anasema hivi: Kutoka upande wa kaskazini nitamuleta Nebukadneza, mufalme wa Babeli, mufalme wa wafalme, akiwa na farasi, magari ya vita, waaskari wapanda-farasi na kundi kubwa, akuje kukushambulia. Ataiangamiza miji inayokuwa jirani yako huko katika vijiji. Kisha atajenga kuta za kukushambulia, atajaza udongo kwenye kuta zako na kuweka ukuta wenye ngao kwa kukushambulia. Ataweka vifaa vyake vya kubomoa mbele ya kuta zako, na kwa nyundo ataivunjavunja minara yako. Farasi wa mufalme Nebukadneza ni wengi na mavumbi watakayorusha juu yatakufunika. Kuta zako zitatetemeka kwa mushindo wa waaskari wapanda-farasi na magari ya vita na ya mizigo wakati atakapoingia kwenye milango yako kama watu wanavyoingia katika muji kupitia pahali palipobomolewa. Kwa kwato za farasi wake, atakanyagakanyaga barabara zako zote. Atawaua watu wako kwa upanga; minara yako mikubwa ataiangusha chini. Ataunyanganya utajiri wako pamoja na biashara yako. Atazibomoa kuta zako na kuziangusha nyumba zako nzuri; mawe, mbao na udongo ulivyotumia kwa kujenga nyumba hizo watavitupa katika bahari. Nitakomesha muziki wa nyimbo zako. Sauti za vinubi vyako hazitasikilika tena. Nitakufanya kuwa kama jiwe; utakuwa pahali pa wavuvi pa kukaushia nyavu zao, wala hautajengwa tena. Mimi Yawe nimesema. –Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe. Bwana wetu Yawe anasema hivi kwa Tiro: Wakaaji wa sehemu za kandokando ya bahari watatetemeka watakaposikia kishindo cha kuanguka kwako na mulio wa maumivu na wa watu wanaouawa. Wakubwa wote wa mataifa ya kandokando ya bahari watashuka toka kwenye viti vyao vya kifalme, na kuvua nguo zao za heshima pamoja na nguo zao zilizopindwa. Kisha kujaa hofu, wataikaa chini; nao watatetemeka wakati wote na kushangaa sana juu ya hayo yaliyokupata. Watakuimbia wimbo huu wa kuomboleza: Namna gani wewe muji wenye utukufu, umetoweka kutoka katika bahari! Ulikuwa na nguvu juu ya bahari, wewe pamoja na wakaaji wako, wewe uliyeletea woga juu ya wote! Sasa watu wa visanga wanatetemeka kwa sababu ya kuanguka kwako; watu wa visanga katika bahari wanatishwa kwa kuanguka kwako! Maana, Bwana wetu Yawe anasema hivi: Nitakufanya wewe Tiro kuwa matongo, kama miji isiyokuwa na watu, nitakapoleta juu yako maji kutoka vilindi vya bahari, na maji mengi yatakufunika. Nitakuteremusha ndani ya shimo kusudi ujiunge na wale wanaokuwa huko, walioishi zamani katika dunia; utakaa kule katika matongo kwa milele. Hautakaliwa na watu milele na hautakuwa na nafasi katika inchi za wanaokuwa wazima. Nitakufanya kuwa kitu cha kuogopesha na itakuwa mwisho wako; watu watakutafuta, lakini hawatakupata tena. –Ni Bwana wetu Yawe anayesema hivyo. Neno la Yawe lilinifikia kusema hivi: Sasa ewe mwanadamu, imba wimbo huu wa maombolezo juu ya muji wa Tiro. Muji wenye kuwa karibu ya bahari, unaofanya biashara na mataifa ya visanga vingi. Umwambie: Bwana wetu Yawe anasema hivi: Ewe Tiro, wewe umejivuna kuwa muzuri kwelikweli! Mipaka yako imeenea kwelikweli! Umejengwa kama mashua nzuri. Waliokujenga walitumia miti ya misunobari ya kutoka Seniri kwa kupasua mbao zako zote; walitwaa mierezi kutoka Lebanoni kwa kukutengenezea mulingoti. Walitwaa miti ya mialo toka Basani wakakuchongea makasia; walikutengenezea mbao za kuikalia kwa miti ya misunobari ya kisanga cha Kipuro, na kuipamba kwa pembe ya tembo. Kitani kilichopindwa vizuri kutoka Misri kilikuwa kwa kupamba tanga lako na kwa ajili ya bendera yako. Chandarua chako kilitengenezwa na nguo ya rangi ya samawi na nyekundu-nyeusi kutoka visanga vya Elisa. Watu wa miji Sidona na Arwadi walikuwa wapiga makasia wako. Wenye hekima wako walikuwa ndani wakifanya kazi ya kuongoza. Wazee wa Gebali na wafundi wao walikuwa wakiziba nyufa zako. Wachuuzi wa bahari waliokuwa wakipitia kwako walifanya biashara nawe. Watu kutoka Persia, Ludi na Puti walijiunga katika kundi lako la waaskari; walilundika ngao zao na kofia zao kwenye kambi zao za kiaskari. Waaskari hao walikupatia utukufu. Watu wa Arwadi pamoja na waaskari wako walilinda kuta zako pande zote, nao watu wa Gamadi walilinda minara yako. Walitundika ngao zao kwenye kuta zako pande zote, na hivyo wakaukamilisha uzuri wako. Watu wa Tarsisi walifanya biashara nawe kwa sababu ya utajiri wako mwingi na wa kila namna. Walitoa feza, chuma, bati, na risasi kwa kupata biashara yako. Watu wa Yavani, Tubali na Meseki, walifanya biashara nawe, wakakupatia watumwa na vifaa vya shaba wapate vitu vyako. Uliuzisha biashara yako huko Beti-Togarma kwa kujipatia farasi wa kubeba mizigo na farasi wa vita, ngamia na nyumbu. Watu wa Dedani walifanya biashara nawe. Inchi nyingi za kandokando ya bahari zilikuwa masoko yako makubwa. Watu wake walikuletea pembe za tembo na miti mizuri inayoitwa ebene kwa kununua vitu kwako. Watu wa Edomu walifanya biashara nawe kwa sababu ya wingi wa vitu vyako. Kwa kupata vitu vyako walikupa akiki, vitambaa vya rangi nyekundu-nyeusi, vitambaa vilivyopindwa vizuri, kitani safi, matumbawe na yakuti. Hata watu wa inchi ya Yuda na ya Israeli walifanya biashara nawe; walikupa ngano, mizeituni, tini za kwanzakwanza, asali, mafuta na marasi kwa kununua vitu kwako. Watu wa Damasiki walifanya biashara nawe kwa sababu ya wingi wa vitu vyako; walikupa divai kutoka muji wa Helboni na manyoya meupe ya kondoo. Wedani na Yavani walisafirisha vitu vyako toka muji wa Uzali; hata chuma kilichofuliwa, mudalasini na muchaichai kwa kununua vitu kwako. Watu wa Dedani walifanya biashara nawe kwa kukupatia matandiko ya farasi. Waarabu na wakubwa wote wa inchi ya Kedari walikuwa wachuuzi wako wakubwa katika biashara ya wana-kondoo, kondoo dume na mbuzi. Wachuuzi wa Seba na wa Rama walifanya biashara nawe; walikuletea viungo vya chakula, mawe ya bei kali na zahabu kwa kujipatia vitu vyako safi. Wakaaji wa miji ya Harani, Kane na Edeni na wachuuzi wa Asuria na Kilmadi walifanya biashara nawe. Hao walifanya nawe biashara ya nguo za bei kali, nguo za rangi nyekundu nyeusi zilizopindwa vizuri, nguo za rangi mbalimbali na kamba ngumu zilizosokotwa. Mashua makubwa za Tarsisi ndizo zilikusafirishia vitu vyako. Basi wewe ulikuwa umejaa vitu kama vile mashua katikati ya bahari. Wavuta makasia wako walikupeleka mbali katika bahari. Upepo mukali wa mashariki umekuvunjavunja ukiwa mbali katikati ya bahari. Mali yako, biashara yako, na vitu vyako, waongozi wako wote katika chombo, wafundi wako wa mashua na wachuuzi wako, waaskari wako wote wanaokuwa kwako, pamoja na wasafiri wanaokuwa kwako, vyote vitaangamia ndani ya bahari, siku ile ya kuangamizwa kwako. Kilio cha waongozi wako kitakaposikilika, inchi za kandokando ya bahari zitatetemeka. Halafu wavuta makasia wote wataziacha mashua zao. Waongozi wote wa mashua watakaa inchi kavu. Wataomboleza kwa uchungu wa moyo juu yako, na kulia kwa uchungu mukubwa; watajitupia mavumbi juu ya vichwa vyao na kugaagaa kwenye majivu. Watajinyoa vichwa kwa ajili yako na kuvaa gunia. Watalia kwa uchungu wa moyo juu yako. Wataimba wimbo wa maombolezo juu yako; Nani aliyepata kuangamizwa kama Tiro katikati ya bahari? Vitu vyako vilipofika katika inchi za ngambo, ulitimiza mahitaji ya watu wengi! Kwa wingi wa utajiri wa vitu vyako uliwatajirisha wafalme wa dunia. Lakini sasa umevunjikia ndani ya bahari; umeangamia katika vilindi vya maji. Biashara yako na watu wote waliokuwa ndani yako vimezama pamoja nawe. Wakaaji wote wa visanga wameshangaa sana juu yako; wafalme wao wameogopa sana, nyuso zimekunjamana kwa huzuni. Wachuuzi wa mataifa watakuzomea! Umekuwa kitu cha kuogopesha, na umetoweka kwa milele! Neno la Yawe lilinifikia kusema hivi: Wewe mwanadamu! Umwambie mufalme wa Tiro kwamba Bwana wenu Yawe anasema hivi: Wewe una kiburi cha moyo, na umesema kwamba wewe ni mungu, kwamba umeikalia kiti cha kifalme cha miungu, umekaa mbali huko katika bahari. Lakini, wewe ni mutu tu wala si mungu, ingawa unajiona kuwa na hekima kama mungu. Wewe unajiona mwenye hekima kuliko Danieli, unazani hakuna siri yoyote usiyoijua. Kwa hekima na akili yako umejipatia utajiri, umejikusanyia zahabu na feza ukaziweka katika hazina zako. Kwa werevu wako mukubwa katika biashara umejiongezea utajiri wako, ukakuwa na kiburi kwa ajili ya mali zako! Kwa hiyo Bwana wetu Yawe anasema hivi: Kwa vile unajiona mwenye hekima kama mungu, basi nitakuletea watu wageni, mataifa ya hatari kuliko yote. Wataharibu utukufu wa hekima yako na kuchafua uzuri wako. Watakutumbukiza chini ndani ya shimo, nawe utakufa kifo cha rafla katika kilindi cha bahari. Utaendelea kujiona kuwa mungu mbele ya hao watakaokuua? Katika mikono ya hao watakaokuangamiza, utatambua kwamba wewe ni mutu tu, wala si mungu! Utakufa kifo cha haya kubwa katika mikono ya watu wa mataifa. –Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe. Tena neno la Yawe lilinifikia kusema hivi: Wewe mwanadamu! Imba wimbo wa maombolezo juu ya mufalme wa Tiro. Umwambie kwamba: Bwana wetu Yawe anasema hivi: Wewe mufalme wa Tiro ulikuwa mupaka wa ukamilifu; ulijaa hekima na uzuri kamili. Ulikaa Edeni, bustani ya Mungu. Ulipambwa kwa kila namna ya mawe ya bei kali, akiki, topazi, yaspi, zabarajadi, berili, sardoniki, yakuti samawi, almasi na zumaridi. Ulikuwa na mapambo ya zahabu. Yote uliwekewa tayari siku ulipoumbwa. Nilichagua kerubi kwa kukulinda, uliishi katika mulima wangu mutakatifu na kutembea juu ya mawe yanayometameta. Uliishi maisha makamilifu tangu siku ile ulipoumbwa, mpaka wakati ulipoanza kufanya uovu. Ustawi wa biashara yako ulikujaza ukali, ukatenda zambi. Kwa hiyo nilikufukuza kama muchafu, mbali na mulima wangu mutakatifu. Na yule kerubi aliyekulinda akakufukuzia mbali na mawe yanayometameta. Ulikuwa na kiburi kwa sababu ya uzuri wako. Uliharibu hekima yako kwa sababu ya utukufu wako. Nilikutupa chini kwenye udongo, nikakufanya kuwa kitisho kwa wafalme. Kwa wingi wa mabaya yako na udanganyifu katika biashara yako ulipachafua pahali pako pa kuabudia; kwa hiyo niliwasha moto kwako, nao ukakuteketeza, nami nikakufanya kuwa majivu juu ya inchi, mbele ya wote waliokuangalia. Wote wanaokufahamu kati ya mataifa wameshikwa na mushangao juu yako. Umekuwa kitu cha kuogopesha, na kutoweka kwa milele. Neno la Yawe lilinifikia kusema hivi: Wewe mwanadamu! Ugeukie upande wa Sidona na kutoa unabii juu yake. Sema hivi: Bwana wetu Yawe anasema hivi: Mimi nitapingana nawe Sidona, na kuonyesha utukufu wangu kati yako. Nitakapotimiza hukumu zangu juu yako na kukuonyesha utakatifu wangu, halafu utatambua kwamba mimi ni Yawe. Nitakutumia ugonjwa mukali na umwangaji wa damu utafanyika katika barabara zako. Utashambuliwa kwa upanga toka pande zote na watu wako watakaouawa, watakuwa wengi. Halafu watatambua kwamba mimi ni Yawe. Mungu anasema: Mataifa jirani za Waisraeli ambayo yalikuwa yanawauzi hayataweza tena kuwaumiza Waisraeli kama vile kwa miiba na michongoma. Halafu watajua kwamba mimi ni Bwana wao Yawe. Bwana wetu Yawe anasema hivi: Nitawakusanya na kuwaleta Waisraeli kutoka katika mataifa yote ambamo walisambazwa. Hivyo nitawafanya watu wa mataifa waone kwamba mimi ni mutakatifu. Waisraeli wataishi katika inchi yao ambayo mimi nilimupa mutumishi wangu Yakobo. Watakaa humo kwa salama kabisa; watajenga nyumba na kupanda mizabibu. Wataishi bila hofu maana mataifa jirani zao ambayo yaliwauzi, mimi nitayaazibu. Hapo watatambua kwamba mimi ni Yawe, Mungu wao. Siku ya kumi na mbili ya mwezi wa kumi, mwaka wa kumi tangu tulipopelekwa katika uhamisho, neno la Yawe lilinifikia kusema hivi: Wewe mwanadamu! Ugeuke kuelekea mufalme wa Misri, utoe unabii juu yake na juu ya inchi yote ya Misri. Umwambie kwamba Bwana wetu Yawe anasema hivi: Mimi nitapingana na wewe mufalme wa Misri, wewe mamba unayelala ndani ya muto Nili! Wewe unafikiri kwamba muto Nili ni wako, kwamba wewe ndiwe uliyeufanya! Basi, nitakutia ndoana katika mataya yako, na kuamuru samaki wakwame katika magamba yako. Nitakuvua kutoka huko ndani ya muto. Nitakutupa katika jangwa, wewe na samaki hao wote. Mwili wako utaangukia katika mbuga; wala hakuna atakayekuokota kusudi akuzike. Nimeutoa mwili wako ukuwe chakula cha nyama wakali na ndege. Halafu wakaaji wote wa Misri watatambua kwamba mimi ni Yawe. Waisraeli walikutegemea wewe ee Misri, lakini umekuwa zaifu kama utete. Walipokushika kwa mukono, ulivunjika na kutegua mabega yao. Walipokuegemea ulivunjika na kutetemesha viungo vyao. Kwa hiyo, Bwana wetu Yawe anasema hivi: Nitaleta upanga juu yako na kuwaua watu na nyama wako wote. Kwa sababu umesema kwamba muto Nili ni wako, kwamba ndiwe uliyeufanya, basi, inchi yako, Misri, itakuwa tupu na jangwa. Halafu watu watatambua kwamba mimi ni Yawe. Hakika nitakuazibu wewe na mito yako; kwa hiyo nitaifanya inchi ya Misri kuwa jangwa na tupu toka Migidoli mpaka Sewene hata kwenye mipaka ya Etiopia. Hakuna mutu wala nyama atakayepita huko. Haitakaliwa kwa muda wa miaka makumi ine. Kati ya miji yote iliyoharibika, miji ya Misri itakuwa mitupu kwa miaka makumi ine. Nitawasambaza Wamisri kati ya watu wa mataifa mengine na kuwaeneza katika inchi zingine. Lakini Bwana wetu Yawe anasema hivi: Kisha ile miaka makumi ine nitawakusanya Wamisri kutoka kwa mataifa walimosambazwa. Nitawafanikisha tena Wamisri. Nitawarudisha katika inchi ya Patro, inchi yao ya asili. Huko watakuwa na ufalme usiokuwa na nguvu, ufalme zaifu kuliko falme zote; wala hawataweza kujipandisha juu ya mataifa mengine. Nitawafanya Wamisri wakuwe watu zaifu hata wasiweze kuyatawala mataifa mengine tena. Misri haitakuwa tena na nguvu za kuweza kutegemewa na Waisraeli. Waisraeli watakumbuka jinsi walivyokosa kwa kutegemea inchi ya Misri. Waisraeli watatambua kwamba mimi ni Bwana wao Yawe. Siku ya kwanza ya mwezi wa kwanza, mwaka wa makumi mbili na saba tangu tulipopelekwa katika uhamisho, neno la Yawe lilinifikia kusema hivi: Wewe mwanadamu! Nebukadneza, mufalme wa Babeli, aliwalazimisha waaskari wake kufanya kazi ngumu ya kuishambulia Tiro. Vichwa vyote vya waaskari wake vilipata upaa na mabega yote yalichubuka. Lakini yeye, wala waaskari wake, hawakupata chochote kutokana na kazi hiyo aliyoifanya juu ya Tiro. Kwa hiyo, Bwana wetu Yawe anasema hivi: Nitamupa Nebukadneza mufalme wa Babeli, inchi ya Misri. Atanyanganya mali yake yote, na kutwaa utajiri wa Misri kuwa mushahara wa waaskari wake. Nimemupa inchi ya Misri kuwa mushahara wa jasho lake kwa maana waaskari wake walifanya kazi kwa ajili yangu. –Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe.– Siku hiyo, nitawafanya Waisraeli wakuwe na nguvu na kukuwezesha wewe Ezekieli useme kati yao. Nao watapata kujua kwamba mimi ni Yawe. Neno la Yawe lilinifikia kusema hivi: Wewe mwanadamu! Toa unabii useme hivi: Bwana wetu Yawe anasema hivi: Muomboleze na kusema: Ole kwetu siku ile! Kwa maana, siku hiyo imekaribia; siku ile ya Yawe iko karibu. Hiyo itakuwa siku ya mawingu ya kutisha, siku ya maangamizi kwa mataifa. Vita itakuja katika inchi ya Misri, na wasiwasi utakuwa katika inchi ya Etiopia, wakati Wamisri wengi wataanguka wameuawa, mali zao zitakaponyanganywa, na misingi ya miji yao kubomolewa. Watu wote waliofungamana na Wamisri, ni kusema watu wa Etiopia, Puti, Ludi, Uarabu yote na Libya wataangamia pamoja nao. Yawe anasema hivi: Wote wanaounga Misri mukono wataangamia, mashujaa wake wenye utukufu wataangamizwa, tangu Migidoli mpaka Sewene watu watauawa katika vita. –Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe.– Misri itakuwa jangwa kama inchi zinazokuwa jangwa na miji yake itakuwa mabomoko kama vile miji iliyoteketezwa. Nitakapoiteketeza Misri kwa moto na kuvunjavunja wasaidizi wake wote, halafu watatambua kwamba mimi ni Yawe. Siku hiyo, nitapeleka wajumbe kwenda kuwatisha Waetiopia wanaojizania kuwa na usalama. Watatetemeka siku Misri itakapoangamia. Kweli! Kweli siku hiyo inakuja! Bwana wetu Yawe anasema hivi: Nitamutumia Nebukadneza, mufalme wa Babeli, kwa kukomesha utajiri wa inchi ya Misri. Nebukadneza mwenyewe pamoja na watu wake, taifa la hatari kuliko mataifa yote, watatumwa kuiangamiza inchi ya Misri. Watachomoa panga zao juu ya Misri na kuijaza inchi hiyo watu waliouawa. Nitaukausha muto Nili na vijito vyake, na kuuzisha inchi ya Misri katika mikono ya watu waovu. Nitasababisha uharibifu katika inchi yote kwa mukono wa watu wageni. Ni Mimi Yawe ninayesema hivyo. Bwana wetu Yawe anasema hivi: Nitaharibu sanamu za miungu, na kukomesha miungu ya uongo ya muji wa Nofi. Hakutakuwa mukubwa tena huko Misri. Nitasababisha hofu itawale katika inchi ya Misri. Muji wa Patro nitaufanya kuwa tupu, muji wa Soani nitauteketeza kwa moto, nitauazibu muji wa No. Nitamwanga kasirani yangu juu ya Sini, ile kimbilio inayotegemewa na Misri; na kuangamiza makundi ya watu wa No. Nitateketeza inchi ya Misri kwa moto. Sini utashikwa na wasiwasi mukubwa, ukuta wa Nofi utabomolewa, nao Nofi utashambuliwa na waadui muchana wazi. Vijana wanaume wa Oni na Pibeseti watauawa kwa upanga, na wakaaji wengine watapelekwa katika uhamisho. Huko Tapanesi muchana utakuwa giza wakati nitakapovunja mamlaka ya Misri na kiburi chake kikubwa kitakapokomeshwa. Wingu litaifunika inchi ya Misri na watu wake watakamatwa mateka. Ndivyo nitakavyoiazibu Misri. Na watu watatambua kwamba mimi ni Yawe. Siku ya saba ya mwezi wa kwanza, mwaka wa kumi na mumoja tangu tulipopelekwa katika uhamisho, neno la Yawe lilinifikia kusema hivi: Wewe mwanadamu! Nimeuvunja mukono wa Mufalme wa Misri, nao haukutunzwa na dawa kusudi uweze kupona na kuweza kushika upanga. Kwa hiyo, Bwana wetu Yawe anasema hivi: Nitapingana na Mufalme wa Misri. Nitaivunja mikono yake yote miwili, ule muzima na hata ule uliovunjika. Na upanga unaokuwa katika mukono wake utaanguka chini. Nitawasambaza Wamisri kati ya mataifa na kuwaeneza katika inchi zingine. Nitaitia mikono ya mufalme wa Babeli nguvu na kutia upanga wangu katika mukono wake. Lakini nitaivunja mikono ya Mufalme wa Misri, naye atalalamika mbele ya mufalme wa Babeli kama mutu aliyeumizwa vibaya sana. Nitaimarisha mikono ya Mufalme wa Babeli, lakini mikono ya Mufalme wa Misri itaregea. Hapo watu watatambua kwamba mimi ni Yawe. Nitakapotia upanga wangu katika mukono wa Mufalme wa Babeli, ataunyoosha juu ya inchi ya Misri kwa kuiazibu, nami nitawasambaza Wamisri kati ya mataifa mengine na kuwaeneza katika inchi zingine. Halafu watatambua kwamba mimi ni Yawe. Katika siku ya kwanza ya mwezi wa tatu, mwaka wa kumi na mumoja tangu tulipopelekwa katika uhamisho, neno la Yawe lilinifikia kusema hivi: Wewe mwanadamu! Umwambie Mufalme wa Misri na watu wake wote hivi: Wewe unafanana na nini kwa ukubwa wako? Wewe ni kama muti wa mwerezi wa Lebanoni wenye matawi mazuri na majani mengi na shina refu. Kilele chake kinafika hata katika mawingu. Maji yaliustawisha, vilindi vya maji viliulisha. Mito ilibubujika pahali ulipoota, ikapeleka vijito kwenye miti yote ya pori. Kwa hiyo, ulirefuka sana kupita miti yote katika pori; matawi yake yalizidi kuwa mengi na makubwa, kutokana na maji mengi ndani ya mizizi yake. Ndege wote waliweka chicha katika matawi yake, nyama wa pori walizalia chini yake, mataifa yote makubwa yalikaa chini ya kivuli chake. Ulikuwa muzuri kwa ukubwa wake, na kwa urefu wa matawi yake. Mizizi yake ilipenya chini mpaka penye maji mengi. Kati ya miti ya mierezi ya bustani ya Mungu, hakuna muti uliolingana nao, wala misunobari haikulingana na matawi yake, mibambakofi haikuwa na matawi kama yake, hata muti wowote wa bustani ya Mungu haukulingana nao kwa uzuri. Mimi niliufanya kuwa muzuri kwa matawi yake mengi; ulionewa wivu na miti yote ya Edeni iliyokuwa katika bustani ya Mungu. Kwa hiyo, Bwana wetu Yawe anasema hivi: Kwa sababu ulirefusha kimo chake na kufikisha kilele chake katika mawingu makubwa, ukajivunia urefu wake, nitautia katika mikono ya mukubwa kati ya mataifa. Yeye, atauazibu. Nimeutupilia mbali kadiri ya uovu wake. Watu wa mataifa mengine ya hatari sana, wataukata na kuuangusha chini na kuulalisha chini. Matawi yake yataanguka chini kwenye mulima na kila pahali katika mabonde; yatavunjika na kulala chini katika mitelemuko yote. Watu wote wataondoka chini ya kivuli chake na kuuacha. Ndege wote watatua juu ya mabaki yake na nyama wote wa pori watakanyaga matawi yake. Hayo yameupata kusudi muti wowote unaokuwa pahali penye maji usiweze kurefuka tena kwa kimo hicho wala kukifikisha kilele chake katika mawingu. Muti wowote unaokunyweshwa maji usiweze tena kufikia urefu huo. Kwa maana kila kitu mwisho wake ni kifo; hata na watu vilevile. Wote watashiriki hali ya wanaoshuka katika shimo kwa wafu. Kwa hiyo Bwana wetu Yawe anasema hivi: Siku ileile muti wa mwerezi ulipofika katika kuzimu nilitandaza giza nene juu yake, nikaufunika; mito yake niliikausha na mutiririko wa maji yake mengi nikaukomesha. Nayo Lebanoni niliiweka katika giza kwa ajili yake, na miti yote katika pori ikazimia kwa ajili yake. Niliyafanya mataifa yatetemeke kwa sauti ya kuanguka kwake, wakati nilipouangusha chini katika kuzimu pamoja na wale wanaoshuka ndani ya shimo kwa wafu. Nayo miti yote ya Edeni, miti mizuri na ya pekee ya Lebanoni ambayo ilimwangiliwa maji, ilifarijiwa huko chini kwa wafu. Hiyo nayo ilishuka kule katika kuzimu pamoja nao, ikajiunga na wale waliofungamana nao na ambao waliikaa chini ya kivuli chake. Kwa uzuri na ukubwa wa muti huo, hakuna muti wowote katika bustani ya Edeni ambao uliweza kulinganishwa nao. Sasa, muti huo ni wewe Mufalme wa Misri. Wewe utatupwa chini kwa wafu pamoja na miti ya Edeni. Utalala karibu na wale wasiomujua Mungu na wale waliouawa kwa upanga. Hiyo itakuwa hali yako ewe Mufalme wa Misri, wewe na watu wako. –Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe. Siku ya kwanza ya mwezi wa kumi na mbili, mwaka wa kumi na mbili tangu tulipopelekwa katika uhamisho, neno la Yawe lilinifikia kusema hivi: Wewe mwanadamu! Imba wimbo wa kuomboleza juu ya Mufalme wa Misri. Wewe Mufalme wa Misri unajiona kuwa simba kati ya mataifa, lakini wewe ni kama mamba tu katika maji: unachomoka kwa nguvu kwenye mito yako, unayavuruga maji kwa miguu yako, na kuichafua mito. Bwana wetu Yawe anasema: Nitautupa wavu wangu juu yako, nao watu watakuvua humo kwa wavu wangu. Nitakutupa juu ya inchi kavu, nitakutupa chini juu ya uwanja, nitaleta ndege wote watue juu yako, na kuwashibisha nyama wote wa pori kwa mwili wako. Nitasambaza nyama yako juu ya milima, na kujaza mabonde yote muzoga wako. Nitaikunywesha inchi damu yako mpaka juu ya milima, mashimo yatajaa damu yako. Nitakapokuangamiza, nitazifunika mbingu, nitazifanya nyota kuwa nyeusi, jua nitalifunika kwa mawingu, na mwezi hautatoa mwangaza wake. Nitaifanya miangaza yote mbinguni kuwa giza nitatandaza giza juu ya inchi. –Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe. Nitaihuzunisha mioyo ya watu wengi, nitakapokupeleka katika utumwa kati ya mataifa, katika inchi ambazo hauzijui. Nitayashitusha mataifa mengi kwa habari zako, wafalme wao watatetemeka kwa sababu yako, nitakaponyoosha upanga wangu mbele yao. Watatetemeka kila wakati, kila mutu akiogopea maisha yake, siku ile ya kuangamia kwako. Kwa maana, Bwana wetu Yawe anasema hivi: Upanga wa mufalme wa Babeli utakufuatilia. Watu wako wengi watauawa kwa mapanga ya mashujaa, watu wa hatari kuliko mataifa yote. Watakomesha kiburi cha Misri na kuwaua watu wako wote. Nitawaangamiza nyama wako wote pembeni ya muto Nili. Maji yake hayatavurugwa tena na mutu wala kwato za nyama kuyachafua tena. Hapo nitayafanya maji yake yatulie na kuitiririsha mito yake kama mafuta. –Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe. Nitakapoifanya inchi ya Misri kuwa jangwa na mali yake yote kunyanganywa, nitakapowaua wakaaji wake wote, halafu watatambua kwamba mimi ni Yawe. Huo ndio wimbo wa maombolezo, wanawake wa mataifa watauimba, wataimba juu ya Misri na watu wake wote. –Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe. Siku ya kumi na tano ya mwezi wa kwanza, mwaka wa kumi na mbili tangu tulipopelekwa katika uhamisho, neno la Yawe lilinifikia kusema hivi: Wewe mwanadamu! Uwaombolezee watu wengi wa Misri. Uwapeleke chini kwenye inchi ya wafu pamoja na mataifa mengine yenye nguvu, waende huko pamoja na wanaoshuka chini kwa wafu. Uwaambie: Ninyi ni wazuri kuliko nani? Muende kuzimu mulalishwe pamoja na wasiomujua Mungu! Wamisri wataangamia pamoja na watu waliouawa katika vita. Upanga uko tayari kuangamiza Misri pamoja na watu wake wengi. Wakubwa wenye nguvu pamoja na wasaidizi wao wakiwa huko katika shimo kwa wafu watasema hivi: Wamisri wameshuka chini kwa wafu, wanalala pamoja na watu wasiomujua Mungu, waliouawa katika vita. Asuria iko huko. Makaburi ya waaskari wake yanaizunguka. Wote waliuawa katika vita. Makaburi yao yako sehemu za chini kabisa katika shimo kwa wafu. Waaskari wao wanaizunguka. Wote waliuawa katika vita. Walipokuwa wangali wanaishi, walieneza vitisho vyao katika inchi ya wanaokuwa wazima. Elamu nayo iko huko. Makaburi ya waaskari wake yanaizunguka. Wote waliuawa katika vita. Wakashuka kwenye inchi ya wafu, bila kujua Mungu. Walipokuwa wangali wanaishi, walieneza vitisho vyao katika inchi ya wanaokuwa wazima. Lakini sasa wanapata haya yao pamoja na wale wanaoshuka katika shimo kwa wafu. Elamu imelalishwa kati ya wale waliouawa katika vita. Makaburi yao yanaizunguka. Wote waliuawa katika vita, bila kujua Mungu. Walipokuwa wangali wanaishi, walieneza vitisho vyao katika inchi ya wanaokuwa wazima, na sasa wako wanapata haya yao pamoja na wale wanaoshuka katika shimo kwa wafu. Wanawekwa kati ya wale waliouawa. Mesaki na Tubali ziko huko. Makaburi ya watu wake wote yanazizunguka. Wote waliuawa katika vita, bila kujua Mungu. Walipokuwa wangali wanaishi, walieneza vitisho vyao katika inchi ya wanaokuwa wazima. Hawakuzikwa pamoja na mashujaa wa zamani, ambao walikwenda katika kuzimu kwa wafu wakiwa na silaha zao, mapanga yao chini ya vichwa vyao na ngao zao juu ya miili yao. Mashujaa hao walipokuwa wangali wanaishi walijaza vitisho vyao katika inchi ya wanaokuwa wazima. Basi, ninyi Wamisri mutaangamizwa na kulalishwa kati ya wasiomujua Mungu waliouawa katika vita. Edomu iko huko pamoja na wafalme wake na wakubwa wao wote. Walipokuwa wangali wanaishi walikuwa na nguvu sana, lakini sasa wamelalishwa kwa wafu pamoja na wasiomujua Mungu waliouawa katika vita. Wakubwa wote wa watu wa upande wa kaskazini wako huko vilevile; hata Wasidoni wote walikwenda kujiunga na wafu. Walipokuwa wangali wanaishi, walisababisha vitisho kwa nguvu zao, lakini sasa hao wasiomujua Mungu wamelalishwa chini na haya pamoja na wale waliouawa katika vita. Wanashiriki haya ya wale walioshuka ndani ya shimo kwa wafu. Mufalme wa Misri, atakapowaona hao wote atafarijika kwa ajili ya wingi wa majeshi yake yote. Nilimuwezesha mufalme wa Misri aeneze vitisho katika inchi ya wanaokuwa wazima, lakini sasa yeye mwenyewe pamoja na jeshi lake lote watauawa katika vita na kulalishwa pamoja na wasiomujua Mungu, waliokufa katika vita. –Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe. Neno la Yawe lilinifikia kusema hivi: Wewe mwanadamu! Ongea na wanainchi wenzako, uwaambie hivi: Kama nikileta vita katika inchi fulani, na watu wa inchi hiyo wakimuchagua mumoja wao akuwe mulinzi wao, huyo anapoona waadui wanakuja, atapiga baragumu na kuwaonya watu. Mutu akisikia sauti ya baragumu lakini akizarau onyo hilo, waadui wakikuja na kumwua, yeye mwenyewe atabeba lazima ya kifo chake. Maana aliisikia sauti ya baragumu, akazarau onyo; basi lawama itakuwa juu yake mwenyewe. Lakini kama angejali hilo onyo, angeyaokoa maisha yake. Lakini kama yule mulinzi akiona waadui wanakuja naye hapigi baragumu na watu wakikosa kuonywa juu ya hatari inayokuja, waadui wakikuja na kumwua mutu yeyote kati yao, huyo mutu aliyekufa, atakuwa amekufa kwa kosa lake. Lakini mimi nitamulaumu mulinzi kwa kifo cha mutu huyo. Basi, ewe mwanadamu, nimekuweka kuwa mulinzi wa Waisraeli. Utakaposikia neno kutoka kwangu utawapa onyo langu. Nikimwambia mutu mwovu hivi: Wewe mutu mwovu hakika utakufa; lakini wewe hausemi chochote kwa kumwonya aachane na mwenendo wake, yule mutu atakufa kwa kosa lake; lakini nitakulaumu wewe kwa kifo chake. Lakini ukimwonya mwovu aachane na mwenendo wake, naye haachani na mwenendo wake mubaya, yeye atakufa kwa kosa lake; lakini wewe utakuwa umeyaokoa maisha yako. Ewe mwanadamu! Uwaambie Waisraeli jambo hili: Ninyi munasema: Tumezidiwa na makosa na zambi zetu. Tunaregea kwa sababu yake! Tutaweza namna gani kuishi? Basi, uwaambie: Kama vile ninavyoishi, –ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe– mimi sikifurahii kifo cha mutu mwovu, lakini ninapenda mutu mwovu aachane na mwenendo wake mubaya, apate kuishi. Mugeuke, muachane na mwenendo wenu mubaya, enyi Waisraeli! Kwa nini munataka kufa? Basi, ewe mwanadamu, uwambie wanainchi wenzako hivi: Mutu wa haki akitenda uovu, haki yake haitamwokoa. Na mutu mwovu akiacha kutenda zambi, hataazibiwa. Mutu wa haki akianza kutenda zambi, haki yake haitamwokoa. Mimi ninamwahidi mutu wa haki kwamba ataishi; lakini yeye akiamini kwamba haki yake inatosha, akianza kutenda uovu, matendo yake yote mema ya zamani hayatakumbukwa; atakufa kwa uovu wake. Tena, nikimwambia mutu mwovu kwamba hakika atakufa naye akiacha zambi yake, akianza kutenda mambo yanayokuwa ya haki na sawa, hatakufa. Kama akirudisha rehani na kurudisha kitu alichoiba, akifuata masharti yanayoleta uzima bila kutenda uovu, mutu huyo hakika ataishi. Hatakufa. Zambi zake zote alizotenda hapo mbele hazitakumbukwa; yeye ametenda mambo yanayokuwa ya haki na mema, kwa hiyo hakika ataishi. Wanainchi wenzako wanasema: Kitu anachofanya Yawe si sawa! Lakini ni wao ndio hawafanyi kitu kinachokuwa sawa. Mutu wa haki akiacha haki yake, akianza kutenda uovu, atakufa kwa sababu ya uovu wake. Na mutu mwovu akiacha uovu wake, akianza kutenda mambo ya haki na mema ataishi kwa sababu ya matendo yake mema. Lakini, ninyi munasema: Anachofanya Yawe si sawa! Enyi Waisraeli, mimi nitamuhukumu kila mumoja wenu kadiri ya matendo yake. Siku ya tano ya mwezi wa kumi, mwaka wa kumi na mbili tangu tulipopelekwa katika uhamisho, mutu mumoja aliyetoroka kutoka Yerusalema alikuja kwangu, akasema: Muji Yerusalema umetekwa! Wakati mutu huyo alipofika, ilikuwa asubui. Jana yake magaribi Yawe alikuwa amenijaza uwezo wake nami sikuwa bubu tena, nikaanza kusema. Neno la Yawe lilinifikia kusema hivi: Wewe mwanadamu! Wakaaji waliobaki katika miji iliyoharibiwa katika inchi ya Israeli wanasema: Abrahamu alikuwa peke yake, hata hivyo, alipata kurizi inchi hii. Lakini sisi ni wengi; ni wazi tumepewa inchi hii ikuwe yetu! Basi, uwaambie kwamba Bwana wetu Yawe anasema hivi: Ninyi munakula nyama yenye damu, munaziabudu sanamu za miungu yenu na kumwanga damu! Munazani kwamba mutapewa inchi hii ikuwe yenu? Munategemea silaha zenu, munafanya mambo ya kuchukiza na kila mwanaume kati yenu analala na muke wa jirani yake! Munazani kwamba mutapewa inchi hii ikuwe yenu? Uwaambie hivi: Bwana wetu Yawe anasema hivi: Kama vile ninavyoishi, hao wanaokaa katika miji hiyo inayokuwa mabomoko, wataagamia kwa upanga; anayekuwa katika vijiji nitamutoa akuliwe na nyama wakali; na wale wanaokuwa kwa milima na ndani ya mapango watakufa kwa ugonjwa mukali. Nitaifanya inchi kuwa jangwa na tupu. Nitawaua mashujaa wake wenye kiburi. Milima ya inchi ya Israeli itakuwa jangwa na hakuna mutu atakayepita huko. Kweli, nitakapoifanya hiyo inchi kuwa jangwa na tupu kwa sababu ya mambo yote ya kuchukiza waliyotenda, halafu watatambua kwamba mimi ni Yawe. Yawe aliniambia: Wewe mwanadamu! Wanainchi wenzako wanasema juu yako, wameikaa juu ya kuta na kwenye milango ya nyumba zao na kuambiana: Tuende kusikiliza neno Yawe alilosema! Basi, wanakuja kwako makundi kwa makundi na kuikaa mbele yako kama watu wangu, kusudi wasikie unachosema, lakini hawafanyi unachowaambia wafanye. Wanasema kwamba wana upendo, lakini hayo ni kusema tu; wanachotafuta kwa moyo ni faida yao tu. Kwao, wewe umekuwa tu kama mwimbaji wa kubembeleza mwenye sauti nzuri ikiandamana na muziki safi! Wanayasikia yale unayosema, lakini hawatii hata neno moja. Lakini hayo unayosema yatakapotukia –nayo kweli yatatukia –basi, halafu watatambua kwamba nabii amekuwa kati yao. Neno la Yawe lilinifikia kusema hivi: Wewe mwanadamu! Toa unabii juu ya wachungaji wa inchi ya Israeli. Uwaambie hao wachungaji kwamba: Bwana wetu Yawe anasema hivi: Ole kwenu ninyi wachungaji wa inchi ya Israeli, munaojikulisha ninyi wenyewe tu! Haiwapasi wachungaji kuwakulisha kondoo? Munakunywa maziwa, munavaa nguo za manyoya yao na munawachinja kondoo wanono na kuwakula. Lakini hamuwakulishi hao kondoo. Wanaokuwa zaifu hamukuwatia nguvu, wagonjwa hamukuwatunza, waliovunjika hamukuwafunga kwa kitambaa, waliotangatanga hamukuwarudisha na waliopotea hamukuwatafuta. Lakini mukawatawala kwa kinguvu na kuwatesa. Basi, kwa sababu hao kondoo hawakuwa na muchungaji, walisambazwa na kuwa chakula cha nyama wa pori. Kweli, kondoo walisambazwa, wakatangatanga juu ya milima na vilima. Kondoo walisambazwa katika dunia yote, na hakukukuwa mutu aliyejali juu yao wala kuwatafuta. Basi, musikie vizuri neno la Yawe, enyi wachungaji: Kama vile ninavyoishi, –ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe– nimechoka kuwaona kondoo wangu wamekuwa chakula cha nyama wakali kwa vile hakukukuwa muchungaji; wachungaji wangu hawakuwatafuta kondoo wangu, lakini wamejikulisha wao wenyewe pahali pa kuwakulisha kondoo wangu. Basi, ninyi wachungaji, musikie neno la Yawe. Bwana wetu Yawe anasema hivi: Nitapingana nanyi, enyi wachungaji. Nitawaondoa madaraka ya kuchunga kondoo wangu, wala sitakubali muwachunge tena. Hamutakuwa tena na nafasi ya kufaidika ninyi wenyewe. Nitawaokoa kondoo wangu toka katika makucha yenu, kusudi wasikuwe chakula chenu tena. Basi, Bwana wetu Yawe anasema hivi: Mimi mwenyewe nitawatafuta kondoo wangu na kuwatunza. Kama muchungaji anavyowatafuta kondoo wake waliosambazwa, ndivyo nitakavyowatafuta kondoo wangu. Nitawarudisha kutoka kila pahali waliposambazwa kwa siku yenye mawingu ya hatari na giza nene. Nitawatoa kutoka kwa watu wa mataifa. Nitawakusanya kutoka inchi za mbali na kuwaleta katika inchi yao wenyewe. Nitawachunga juu ya milima ya inchi ya Israeli, kandokando ya vijito na katika sehemu zote za inchi zinazokaliwa na watu. Nitawapa malisho mazuri kwenye milima mirefu ya inchi ya Israeli ambako kuna mashamba mazuri ya kuwakulishia. Watapumzika huko kwenye mbuga za malisho mazuri; watapata malisho mazuri juu ya milima ya inchi ya Israeli. Mimi mwenyewe nitakuwa muchungaji wa kondoo wangu. Mimi mwenyewe nitawapumzisha. –Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe.– Nitawatafuta kondoo waliopotea na waliotangatanga nitawarudisha kwa nyumba. Waliovunjika nitawatunza, na wale wanaokuwa zaifu nitawapatia nguvu. Lakini kondoo wanono na wenye nguvu nitawaangamiza. Mimi nitawachunga kondoo kama inavyostahili. Bwana wetu Yawe anasema hivi: Kwa ninyi munaokuwa kundi langu, nitaamua kati ya kondoo na kondoo; kati ya kondoo dume na mbuzi. Wamoja kati yenu wanakula malisho mazuri na vilevile kukanyagakanyaga yale yaliyobaki. Wanakunywa maji safi na yanayobaki wanayachafua kwa miguu yao! Basi, kondoo wangu wengine wakule malisho yaliyokanyagwakanyagwa na kunywa maji yaliyochafuliwa? Kwa hiyo, Bwana wetu Yawe anasema hivi: Mimi mwenyewe nitaamua kati ya kondoo wanono na kondoo zaifu. Ninyi munawasukuma kwa mbavu na kwa mabega na kuwapiga pembe kondoo wote wanaokuwa zaifu hata mumewatawanya mbali na kundi. Lakini mimi nitawaokoa kondoo wangu wasiendelee tena kuteswa. Nitatoa hukumu juu ya kila kondoo. Nitaweka muchungaji mumoja juu yao, mufalme kama mutumishi wangu Daudi. Yeye atawakulisha na kuwa muchungaji wao. Nami Yawe, nitakuwa Mungu wao, naye mutumishi wangu Daudi atakuwa mukubwa wao. Ni mimi Yawe ninayesema hivyo. Nitafanya nao agano la amani. Nitaondoa nyama wakali katika inchi, kusudi kondoo wangu wakae katika mbuga kwa usalama na kulala katika pori. Nitawafanya waishi kandokando ya mulima wangu mutakatifu na kuwabariki. Nitawaletea mvua kwa wakati wake, nazo zitakuwa mvua za baraka. Miti inayokuwa katika mashamba itazaa matunda, udongo utatoa mazao kwa wingi, nao wataishi kwa salama katika inchi yao. Nitakapovunja nira zao za utumwa na kuwaokoa toka katika mikono ya hao waliowafanya kuwa watumwa halafu watatambua kwamba mimi ni Yawe. Hawatakamatwa tena mateka na mataifa mengine wala nyama wa pori hawatawaua na kuwakula. Wataishi kwa usalama na hakuna atakayewatisha. Nitawapa mashamba yenye mboleo kusudi wasiangamizwe tena na njaa katika inchi ile, wala kuzarauliwa tena na mataifa mengine. Nao watajua kwamba mimi Yawe, Mungu wao, niko pamoja nao na kwamba watu hao wa inchi ya Israeli ni watu wangu. Nanyi, ee kondoo wangu, ninyi ni watu wangu, nami ni Mungu wenu. –Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe. Neno la Yawe lilinifikia kusema hivi: Wewe mwanadamu! Ugeukie upande wa mulima Seiri, utoe unabii juu ya wakaaji wake. Uwaambie kwamba: Bwana wetu Yawe anasema hivi: Mimi ninapingana nawe, ee mulima Seiri. Ninanyoosha mukono wangu juu yako na kukufanya ukuwe jangwa na ukiwa. Ninaifanya miji yako kuwa mabomoko nawe utakuwa jangwa. Halafu utatambua kwamba mimi ni Yawe. Ulikuwa adui wa siku zote wa Waisraeli, ukasababisha watu wake wauawe kwa upanga, wakati wa musiba wao, wakati wa azabu yao ya mwisho. Kwa hiyo, kama vile ninavyoishi, –ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe– kifo kinakungoja na hautaweza kukiepuka. Uko na makosa ya mauaji, basi mauaji nayo yatakuandama. Nitaufanya mulima Seiri kuwa ukiwa na jangwa na yeyote atakayepitia huko nitamwangamiza. Nitajaza milima yako watu waliouawa; na katika vilima vyako na mabonde yako na mitelemuko yako yote kutakuwa watu waliouawa kwa upanga. Nitakufanya kuwa jangwa milele, na miji yako haitakaliwa tena. Halafu utatambua kwamba mimi ni Yawe. Wewe ulisema kwamba mataifa hayo mawili, ni kusema inchi ya Yuda na ya Israeli, ni mali yako na kwamba utazirizi! Ulisema hivyo ingawa humo ni makao yangu mimi Yawe. Kwa hiyo, kama vile ninavyoishi, –ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe– nitakutendea kadiri ya hasira na wivu wako, kulingana na chuki yako kwao. Nitakapokuazibu utatambua mimi ni nani! Wewe utajua kwamba mimi mwenyewe Yawe nimeyasikia matusi yote uliyoyatoa juu ya milima ya Waisraeli, ukisema: Milima ya Israeli imefanywa kuwa jangwa! Imetolewa kusudi tupate kuinyanganya! Nimesikia jinsi unavyojivuna na kusema maneno mengi juu yangu. Bwana wetu Yawe anasema hivi: Nitakapokufanya wewe Edomu kuwa jangwa, dunia yote itafurahi kama wewe ulivyofanya wakati inchi ya Waisraeli ilipoharibiwa. Utakuwa jangwa, ewe mulima Seiri, pamoja na inchi yote ya Edomu. Halafu watu watatambua kwamba mimi ni Yawe. Yawe aliniambia hivi: Wewe mwanadamu! Toa unabii juu ya milima ya Israeli. Uiambie isikilize maneno yangu. Bwana wetu Yawe anasema hivi: Waadui zenu wamewazomea na kusema kwamba ninyi mumekuwa mali yao! Kwa hiyo, wewe Ezekieli, toa unabii useme kwamba Bwana wenu Yawe anasema hivi: Watu wamewafanya ninyi milima ya Waisraeli kuwa tupu na kuwashambulia kutoka kila upande hata mumekuwa mali ya mataifa mengine, mukakuwa kitu cha kusimangwa na kuchekelewa kati ya watu! Kwa hiyo, enyi milima ya Waisraeli, musikie neno la Bwana wenu Yawe. Anasema juu ya ninyi milima na vilima, mifereji na mabonde, jangwa tupu na miji ya matongo, na miji iliyokamatwa mateka na kuzarauliwa na mataifa yote yanayowazunguka. Bwana wenu Yawe anasema hivi: Wivu wangu unawaka sana. Nitayaazibu mataifa mengine na hasa watu wa inchi ya Edomu. Wao kwa furaha ndani ya moyo na mazarau walikamata hiyo inchi inayokuwa yangu ikuwe yao. Kwa hiyo, ewe mwanadamu, toa unabii juu ya inchi ya Waisraeli, uiambie milima na vilima, vijito na mabonde kwamba Bwana wao Yawe anasema hivi: Ninasema kutokana na upendo wangu wenye wivu juu ya ninyi, inchi yangu, kwa sababu mumetukanwa na watu wa mataifa. Bwana wenu Yawe anasema hivi: Ninaapa hakika kwamba watu wa mataifa yanayokuwa jirani yenu watatukanwa wao wenyewe. Lakini juu ya milima ya Waisraeli, miti itatoa matawi na kuzaa matunda kwa ajili ya watu wangu Waisraeli, maana wao wanakaribia kurudi katika inchi yao. Mimi niko upande wenu, nitahakikisha kuwa udongo wenu utalimwa na kupandwa mbegu. Nitawazidisha sana Waisraeli. Miji itakaliwa, na mabomoko yatajengwa upya. Nitawafanya watu na nyama waongezeke na kuwa wengi. Nitawafanya ninyi milima mukaliwe tena kama zamani. Nitawatendea mema mengi kuliko zamani. Nanyi mutatambua kwamba mimi ni Yawe. Nitawafanya watu wangu Waisraeli watembee juu yenu. Nanyi mutakuwa urizi wao, wala hamutawafanya tena wakufiwe na watoto wao. Bwana wetu Yawe anasema hivi: Kwa vile watu wamesema juu yenu kwamba munakula watu, na mumeliteketezea taifa lenu watoto wake, basi, sasa hamutakula tena watu wala kuteketezea taifa lenu watoto wake. Sitaruhusu tena mataifa yawatukane, wala kuwazarau tena. Hamutasababisha taifa lenu kukosa. –Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe. Neno la Yawe lilinifikia kusema hivi: Wewe mwanadamu! Waisraeli walipoishi katika inchi yao waliichafua kwa mienendo na matendo yao. Niliyaona matendo yao kuwa sawa na mwanamuke anayekuwa muchafu wakati wa ugonjwa wake wa mwezi. Niliwamwangia kasirani yangu kwa sababu ya damu waliyomwanga katika inchi na kwa sababu ya miungu ambayo kwa ajili yao waliichafua inchi. Niliwasambaza kati ya mataifa, wakasambazwa katika inchi nyingine. Niliwaazibu kadiri ya tabia yao na matendo yao. Hata walipokuwa kati ya mataifa walilikufuru jina langu takatifu, hata watu wakasema hivi juu yao: Hawa ndio wale watu wa Yawe, lakini wamelazimishwa kuondoka katika inchi yake! Hiyo ilinifanya kuhangaika juu ya jina langu takatifu ambalo Waisraeli walilikufuru kati ya mataifa walikokwenda. Basi, uwaambie Waisraeli kwamba: Bwana wetu Yawe anasema hivi: Ninachotaka kufanya si kwa faida yenu ninyi watu wa inchi ya Israeli, lakini ni kwa heshima ya jina langu takatifu mulilolikufuru kati ya mataifa mulikokwenda. Nitalitakasa jina langu kubwa mulilokufuru kati ya mataifa. Na kwa hiyo mataifa yatatambua kwamba mimi ni Yawe. –Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe.– Nitawatumia ninyi kuonyesha utakatifu wangu mbele yao. Nitawaondoa ninyi katika kila taifa na kuwakusanya kutoka inchi zote za kigeni; nitawarudisha katika inchi yenu wenyewe. Nitawanyunyizia maji safi, nanyi mutakuwa safi. Nitawatakasa toka uchafu wenu wote na toka uchafu wa sanamu za miungu yenu yote. Nitawapa moyo mupya na kuweka roho mupya ndani yenu. Nitauondoa kwenu moyo mugumu kama jiwe na kuwapa moyo musikilivu. Nitatia roho yangu ndani yenu; nitawafanya mufuate masharti yangu na kushika maagizo yangu. Mutakaa katika inchi niliyopatia wazee wenu. Mutakuwa watu wangu, nami nitakuwa Mungu wenu. Nitawaokoa kutoka uchafu wenu wote. Nitaiamuru ngano iongezeke, wala sitawaletea njaa tena. Nitayazidisha matunda ya miti na mazao ya mashamba kusudi musizarauliwe tena kwa ajili ya njaa kati ya mataifa. Kisha mutakapokumbuka mienendo yenu miovu na matendo yenu mabaya, mutajichukia wenyewe kwa sababu ya maovu yenu na machukizo muliyofanya. Lakini mujue kwamba sitafanya hivyo kwa ajili yenu. –Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe.– Lakini mupate haya na kufazaika kwa sababu ya matendo yenu, enyi Waisraeli! Bwana wetu Yawe anasema hivi: Siku ile nitakapowasafisha ninyi toka maovu yenu yote, nitaifanya miji yenu ikaliwe, nayo mabomoko yajengwe upya. Inchi iliyokuwa jangwa italimwa tena, hata atakayepita huko hataiona kuwa jangwa. Nao watu watasema: Inchi hii iliyokuwa jangwa, sasa imekuwa kama bustani ya Edeni, nayo miji iliyokuwa ukiwa, matongo na mabomoko, sasa inakaliwa na watu, tena inazungukwa na kuta! Hapo mataifa yaliyobaki kandokando yenu, yatatambua kwamba ni mimi Yawe niliyejenga upya yaliyoharibiwa na kupanda mbegu katika inchi iliyokuwa jangwa. Ni mimi Yawe ninayesema hivyo, na nitafanya hayo. Bwana wetu Yawe anasema hivi: Waisraeli wataniomba niwafanye kuwa wengi kama kundi la kondoo, nami nitawafanya hivyo. Wataniomba wakuwe wengi kama kundi la kondoo wa kutolewa sadaka, kama kundi la kondoo katika Yerusalema wakati wa sikukuu zake. Hivi ndivyo miji yenu iliyokuwa ukiwa itakavyojaa makundi ya watu. Kwa hiyo watatambua kwamba mimi ni Yawe. Yawe alinijaza uwezo wake mimi Ezekieli. Roho wake akanitwaa na kunipeleka katika bonde lililokuwa limejaa mifupa. Basi, akanitembeza kila pahali katika bonde lile. Kulikuwa mifupa mingi sana katika bonde lile, nayo ilikuwa inakauka kabisa. Yawe akaniuliza hivi: Wewe mwanadamu! Mifupa hii inaweza kuishi tena? Nami nikamujibu: Ee Bwana wetu Yawe, wewe unajua! Naye akaniambia: Toa unabii juu ya mifupa hii. Uiambie hivi: Enyi mifupa yenye kukauka, musikilize neno la Yawe. Bwana wetu Yawe anasema hivi: Nitapulizia tena pumzi ndani yenu, nanyi mutaishi. Nitawatia mishipa na nyama, nitawafunika ngozi na kutia pumzi ndani yenu, nanyi mutaishi. Hapo mutajua kwamba mimi ni Yawe. Basi, nikatoa unabii kama nilivyoamriwa. Nilipokuwa nikitoa unabii, kukatokea kelele kama ya mukwaruzo na ile mifupa ikaanza kusogeleana na kuungana. Niliangalia, nikaona ile mifupa imewekewa mishipa na nyama na kufunikwa kwa ngozi. Lakini haikukuwa na uzima. Halafu, Yawe akaniambia: Ewe mwanadamu, kwa ajili yangu toa unabii kwa upepo, uuambie kwamba Bwana wetu Yawe anasema hivi: Ewe upepo kuja toka pande zote ine na kuipulizia miili hii iliyokufa kusudi ipate kuishi. Basi, mimi nikatoa unabii kama alivyoniamuru, nayo pumzi ikaingia ndani yao, nayo ikapata tena uzima, ikasimama wima: kundi kubwa ajabu. Kwa hiyo Yawe akaniambia: Wewe mwanadamu! Mifupa hiyo ni mufano wa watu wote wa inchi ya Israeli. Wao, wanasema: Mifupa yetu imekauka, matumaini yetu yamepotea nasi tumekwisha kabisa. Kwa hiyo, toa unabii, uwaambie kwamba Bwana wenu Yawe anasema hivi: Enyi watu wangu, nitayafunua makaburi yenu na kuwafufua kutoka ndani ya makaburi yenu. Nitawarudisha ndani ya nyumba zenu katika inchi ya Israeli. Nanyi, enyi watu wangu, mutatambua kwamba mimi ni Yawe nitakapofunua makaburi yenu na kuwafufua kutoka ndani ya makaburi yenu. Nitatia Roho yangu ndani yenu, nanyi mutaishi, nami nitawaweka katika inchi yenu wenyewe. Kwa hiyo mutatambua kwamba mimi Yawe nimesema, nami nitafanya hayo. Ni mimi Yawe ninayesema hivyo. Neno la Yawe lilinifikia kusema hivi: Wewe mwanadamu, twaa kijiti kimoja, uandike juu yake maneno haya: Kwa Yuda na Waisraeli wanaoshirikiana naye. Kisha twaa kijiti kingine uandike juu yake maneno haya: Kwa Yosefu (kijiti cha Efuraimu) na Waisraeli wanaoshirikiana naye. Halafu uvitwae vijiti hivyo na kuvishikamanisha kusudi vionekane kama kijiti kimoja. Wanainchi wenzako watakuuliza: Hautatuelezea maana ya jambo hilo? Wewe utawajibu: Bwana wetu Yawe anasema hivi: Nitakitwaa kijiti cha Yosefu (kinachokuwa katika mukono wa Efuraimu) na makabila ya Israeli yanayoungana naye, nami nitakishikamanisha na kijiti cha Yuda kusudi vijiti hivyo viwili vifanywe kijiti kimoja katika mukono wangu. Utakamata vile vijiti ulivyoandika juu yake katika mukono wako kwa jinsi kila mutu apate kuona, uwaambie kwamba Bwana wetu Yawe anasema hivi: Nitawatoa Waisraeli kutoka mataifa walikokwenda; nitawakusanya toka pande zote na kuwarudisha katika inchi yao. Nitawafanya kuwa taifa moja katika inchi juu ya milima ya Israeli; mufalme mumoja atakuwa mufalme wao wote. Hawatakuwa tena mataifa mawili wala hawatagawanyika tena kuwa falme mbili. Hawatajichafua tena kwa kuabudu sanamu za miungu yao na kwa mambo yao ya kuchukiza wala kwa makosa yao. Nitawaokoa wasikuwe tena waasi. Nao watakuwa watu wangu nami nitakuwa Mungu wao. Mutumishi wangu Daudi atakuwa mufalme wao; watakuwa na muchungaji mumoja tu. Watayafuata maagizo yangu na kushika masharti yangu. Watakaa katika inchi ya wazee wao ambayo nilimupa Yakobo. Wao na watoto wao na wajukuu wao wataishi humo milele. Naye Daudi, mutumishi wangu, atakuwa mutawala milele. Nitafanya nao agano la amani, nalo litakuwa agano la milele. Nitawabariki na kuwafanya wakuwe wengi, nami nitaweka hekalu langu kati yao milele. Nitaishi kati yao; nitakuwa Mungu wao nao watakuwa watu wangu. Nayo mataifa yatatambua kwamba mimi Yawe, nimewatakasa Waisraeli na kwamba hekalu langu liko kati yao milele. Neno la Yawe lilinifikia kusema hivi: Wewe mwanadamu! Umugeukie Gogi mufalme wa inchi ya Magogi ambaye ni mutawala mukubwa wa Meseki na Tubali. Toa unabii juu yake na kumwambia kwamba: Bwana wetu Yawe anasema hivi: Mimi nitapingana nawe, ewe Gogi, mutawala wa Meseki na Tubali. Mimi nitakugeuza na kukutia ndoana katika mataya yako, na kukutoa inje wewe pamoja na kundi lako lote la waaskari: farasi na waaskari wapanda-farasi na kundi kubwa la watu wanaovaa nguo za vita, ngao kubwa na ndogo katika mikono pamoja na mapanga yao. Kati yao kuna waaskari kutoka Persia, Etiopia na Puti; wote wana ngao na kofia za chuma. Vilevile makundi ya waaskari kutoka Gomeri, Beti Torgama, upande wa kaskazini kabisa, na makundi yao yote pamoja na makundi kutoka katika mataifa mengine, yako pamoja nawe. Ujitayarishe, uikae wewe mwenyewe na kundi lako lote pamoja na wengine wote unaokuwa nao, uwalinde. Kisha siku nyingi utaitwa kuishambulia inchi ambayo watu wengi waliletwa kutoka mataifa mengi na sasa wanaishi bila vitisho vya vita. Utaishambulia milima ya Israeli ambayo hapo zamani ilikuwa jangwa na matongo kwa muda murefu, lakini sasa watu wote huko wanaishi kwa usalama. Utakwenda mbio kama zoruba na kuifunika inchi kama wingu, wewe mwenyewe na kundi lako lote la waaskari pamoja na mataifa mengi yanayokuwa pamoja nawe. Bwana wetu Yawe anasema hivi: Siku ile, utaanza kuwaza ndani ya moyo wako na kupanga mipango miovu na kusema: Nitakwenda kuishambulia inchi isiyokuwa na kuta, inchi ambako wanainchi wake wanaishi kwa amani. Wote wanakaa katika miji isiyokuwa na kuta; hawana vifungio wala milango. Utanyanganya na kuteka mali za watu wanaokaa katika miji ambayo ilikuwa jangwa. Watu hao wamekusanywa kutoka katika mataifa na sasa wana makundi ya nyama na mali; nao wanakaa kwenye kitofu cha dunia. Wakaaji wa Seba na Dedani pamoja na wachuuzi wa Tarsisi na wa vijiji vyake watakuuliza: Umekuja kunyanganya? Umekusanya kundi lako la waaskari kwa kushambulia na kutwaa mateka na kubeba feza na zahabu, makundi ya nyama na vitu, na kuondoka na vitu vingi? Kwa hiyo, ewe mwanadamu, toa unabii na kumwambia Gogi kwamba Bwana wenu Yawe anasema hivi: Siku ile, taifa langu la Waisraeli litaishi kwa usalama, wewe utafunga safari kutoka kwenye makao yako, huko mbali kabisa upande wa kaskazini, ukuje pamoja na watu wengi wakiwa wote wamepanda farasi: jeshi kubwa na lenye nguvu. Utawashambulia Waisraeli, kama vile wingu linalotanda juu ya inchi. Wakati huo nitakutuma uishambulie inchi yangu, kusudi mataifa yajue kwamba nimekutumia wewe Gogi kusudi nionyeshe utakatifu wangu mbele yao. Bwana wetu Yawe anasema hivi: Wewe ndiwe niliyesema habari zako hapo zamani kwa njia ya watumishi wangu manabii wa Israeli, ambao walitabiri nyakati zile kwamba nitakuleta kusudi ushambulie watu wa Israeli. Siku ile Gogi atakapoishambulia inchi ya Israeli, nitawakisha kasirani yangu. –Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe.– Mimi ninasema wazi kwa wivu na kasirani yangu kali kwamba siku hiyo kutakuwa tetemeko kubwa la inchi katika inchi ya Israeli. Samaki na ndege, nyama wa pori, viumbe vyote vinavyotambaa pamoja na watu wote katika dunia, watatetemeka kwa kuniona. Milima itaporomoshwa, mawe yataanguka na kuta zote zitaanguka chini. Nami nitasababisha kila namna ya kitisho juu ya Gogi. –Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe.– Waaskari wake wataanza kushambuliana wenyewe kwa mapanga yao. Nitamwazibu Gogi kwa ugonjwa mukali na mauaji. Nitanyesha mvua nyingi na mvua ya mawe na moto na kiberiti juu yake, juu ya makundi yake, na mataifa yale mengi yanayokuwa pamoja naye. Ndivyo nitakavyofanya kusudi yote yaone ukubwa wangu na utakatifu wangu. Halafu watatambua kwamba mimi ni Yawe. Bwana wetu Yawe akaniambia: Wewe mwanadamu! Toa unabii juu ya Gogi. Useme: Bwana wetu Yawe anasema hivi: Mimi nitapingana nawe Gogi mutawala mukubwa wa mataifa ya Meseki na Tubali. Nitakugeuza na kukuelekezea upande mwingine na kukuongoza kutoka mbali upande wa kaskazini uende kushambulia milima ya Israeli. Kisha nitauvunja upinde wako katika mukono wako wa kushoto, na mishale yako katika mukono wako wa kuume nitaiangusha chini. Utakufa juu ya milima ya Israeli, wewe pamoja na makundi yako yote ya waaskari na mataifa yanayokuwa pamoja nawe. Nami nitaitoa miili yao ikuliwe na ndege wa kila aina na nyama wakali. Utakufia katika pori. –Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe.– Nitawasha moto juu ya inchi ya Magogi na juu ya wote wanaokaa salama katika inchi za kandokando ya bahari. Nao watatambua kwamba mimi ni Yawe. Nitajulisha jina langu takatifu kwa watu wangu Waisraeli, wala sitaruhusu tena watu walikufuru jina langu takatifu. Nayo mataifa yatatambua kwamba mimi ni Yawe, Mutakatifu wa Israeli. Siku ile ninayosema juu yake, kwa hakika inakuja. –Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe.– Kwa hiyo, watu wanaoishi katika miji ya Israeli watatoka na kukusanya silaha zilizoachwa na kuzichoma kwa moto. Watatumia hizo ngao, pinde, mishale, mikuki na magongo, kama kuni za kuwasha moto kwa muda wa miaka saba. Hawatahitaji kuokota kuni katika mashamba, wala kukata miti katika pori, kwa sababu watazitumia hizo silaha kwa kuwasha nazo moto. Watabeba mali za wale walioteka mali zao na kuwanyanganya mali zao. –Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe.– Katika siku ile, nitamupa Gogi pahali pa kufanyia maziko katika inchi ya Israeli, katika Bonde la Wasafiri, upande wa mashariki wa bahari ya Chumvi. Gogi atazikwa huko pamoja na kundi lake lote la waaskari, nao wasafiri watazuizwa kupita kule. Bonde hilo litaitwa, Bonde la Hamoni-Gogi. Kwa kuisafisha inchi, Waisraeli watatumia muda wa miezi saba kuzika maiti hizo. Watu wote katika inchi watashugulika na kuwazika. Na hilo litakuwa jambo la kuwapatia sifa, siku ile nitakapoonyesha utukufu wangu. –Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe.– Kisha miezi hiyo saba, watatenga watu watakaopitapita katika inchi kwa kutafuta maiti ambazo zitakuwa bado hazijazikwa, wazizike kwa kuisafisha inchi. Wanapoona mufupa wa mutu wataweka kitambulisho juu yake kusudi wale wanaozika wakuje na kuuzika katika Bonde la Hamoni-Gogi. Huko kutakuwa vilevile muji utakaoitwa “Muji wa watu wengi”. Ndivyo watakavyoisafisha inchi. Sasa, ewe mwanadamu, Bwana wetu Yawe anasema hivi: Uite ndege wote na nyama wote wa pori wakusanyike toka pande zote na kuja kukula karamu ya sadaka ya nyama ninayowatayarishia, ambayo itakuwa kubwa sana juu ya milima ya Israeli, ambako watakula nyama na kunywa damu. Watakula nyama ya mashujaa, watakunywa damu ya wakubwa wa dunia watakaochinjwa kama kondoo dume au wana-kondoo, mabeberu au ngombe dume wanono wa Basani. Katika karamu hiyo niliyowafanyia watakula mafuta na kushiba. Watakunywa damu na kulewa. Kwenye meza yangu, watashibishwa kwa farasi, waaskari wapanda-farasi, mashujaa na watu wote wa vita. –Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe. Yawe akaniambia hivi: Nitaonyesha utukufu wangu kwa mataifa yote, na kuwaonyesha jinsi ninavyotumia nguvu yangu kwa kutimiza hukumu zangu za haki. Waisraeli watajua kwamba mimi ni Yawe, Mungu wao, tangu siku hiyo na itakayokuja. Mataifa yatajua kwamba Waisraeli walikwenda katika uhamisho kutokana na makosa yao wenyewe waliyonikosea. Waliniasi, nami nikageuka wasipate kuniona, nikawatoa katika mikono ya waadui zao wakauawa. Niligeuka wasipate kuniona nikawatendea kulingana na uchafu na makosa yao. Kwa hiyo Bwana wetu Yawe anasema hivi: Sasa nitawahurumia Waisraeli wazao wa Yakobo, na kuwarudishia fanaka yao. Ninataka jina langu takatifu liheshimiwe siku zote. Watakapokuwa wanaishi kwa usalama katika inchi yao, bila kutishwa, watasahau haya yao na uasi walionitendea. Wakati huo, nitakuwa nimewarudisha kutoka kwa mataifa na kuwakusanya kutoka inchi za waadui zao na kuonyesha utakatifu wangu mbele ya mataifa mengi. Kisha watatambua kwamba mimi ni Yawe, Mungu wao, kwa sababu mimi niliwapeleka katika uhamisho kati ya mataifa na kuwarudisha tena katika inchi yao. Sitamwacha hata mutu wao mumoja abakie kati ya mataifa. Nitakapowajaza Waisraeli Roho yangu, sitageuka tena wasipate kuniona. –Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe.– Katika mwaka wa makumi mbili na tano tangu tulipopelekwa katika uhamisho, siku ya kumi ya mwezi wa kwanza, siku hiyo Yawe alinijaza uwezo wake. Ilikuwa mwaka wa kumi na ine tangu pale Yerusalema ulipotekwa. Basi, nikiwa katika maono Yawe akanipeleka mpaka katika inchi ya Israeli, akaniweka juu ya mulima murefu sana, na upande wa kusini kulikuwa majengo yaliyoonekana kama muji. Basi, alinipeleka huko, nami nikamwona mutu aliyeonekana anaangaa kama shaba. Katika mikono yake mutu huyo alikuwa na kamba ya kitani ya kupima nayo pamoja na ufito wa kupima nao, naye alikuwa amesimama karibu na mulango. Basi, akaniambia hivi: Wewe mwanadamu! Angalia vizuri na kusikiliza kwa uangalifu. Shika kwa moyo uone kila kitu nitakachokuonyesha maana umeletwa hapa kusudi nikuonyeshe kitu. Unapaswa kuwatangazia watu wa Israeli kila kitu utakachoona. Basi, huko, niliona hekalu nalo lilikuwa limezungukwa na ukuta upande wa inje. Yule mutu akatwaa ufito wake wa kupima ambao ulikuwa na urefu kwenda juu wa metre tatu, akapima ule ukuta. Ukuta huo ulikuwa na kimo cha metre tatu na unene wa metre tatu. Kisha, akaenda kwenye mulango wa upande wa mashariki akapanda juu ya ngazi naye akiwa juu akapima kizingiti cha mulango ambacho kilikuwa na upana wa metre tatu. Kulikuwa vyumba vya walinzi kila upande wa nafasi ya kupitia na kila kimoja kilikuwa cha muraba: urefu metre tatu upana metre tatu. Kuta zilizotenganisha vyumba hivyo zilikuwa na unene metre mbili na nusu. Kulikuwa baraza ya urefu wa metre tatu ambao ulielekea kwenye chumba kikubwa mbele ya hekalu. Yule mutu akakipima vilevile chumba hicho, nacho kilikuwa na upana wa metre ine. Halafu akapima kuta zake za inje zikaonekana zina unene wa metre moja. Sehemu ya ndani ya mulango ilikuwa sehemu iliyokuwa karibu zaidi na hekalu. Kulikuwa sehemu ya kuingilia iliyokuwa na vyumba vitatu vya walinzi, kila upande na vyote vilikuwa na ukubwa uleule; nazo kuta zilizovitenganisha zilikuwa na unene uleule. Kisha, yule mutu akapima upana wa nafasi ya kupitia katika mulango. Upana wake ulikuwa metre sita na nusu. Ukubwa wote wa baraza ya katikati ya kupitia ulikuwa metre tano. Mbele ya vyumba vya walinzi ambavyo vilikuwa muraba: metre tatu kwa tatu, kulikuwa ukuta mufupi kama kizuizi ukiwa na kimo cha sentimetre makumi tano na unene sentimetre makumi tano. Yule mutu akapima hatua kutoka ukuta wa nyuma wa chumba kimoja mpaka kwenye ukuta wa nyuma ya chumba upande wa pili penye nafasi ya kupitia, akapata metre kumi na mbili na nusu. Chumba cha mwisho kabisa kilielekea kwenye kiwanja. Akakipima chumba hicho nacho kilikuwa na upana metre kumi. Kutoka mbele ya mulango kwenye kiingilio mpaka kwenye baraza la ndani la mulango kulikuwa metre makumi mbili na tano. Kulikuwa matundu madogomadogo kwenye miimo ya inje ya vyumba vyote na hata kwenye kuta zilizotenganisha vyumba. Kulikuwa michoro ya miti ya ngazi kwenye miimo ya ndani iliyoelekea baraza la kupitia. Kisha yule mutu akanipeleka mpaka katika kiwanja cha inje cha hekalu. Huko kulikuwa vyumba makumi tatu vyenye kuuzunguka ukuta wa inje na mbele ya vyumba hivyo kulikuwa sakafu ya mawe. Sakafu hiyo ilitandazwa kuzunguka milango kwa kufuatana na urefu wa milango hiyo; hiyo ilikuwa sakafu ya chini. Kisha, yule mutu akapima hatua ya njia iliyokuwa ikitoka kwenye kiwanja cha ndani cha sehemu ya chini ikielekea inje ya kiwanja hicho, akapata metre makumi tano. Kisha, yule mutu akapima urefu na upana wa mulango wa upande wa kaskazini na kiwanja cha inje. Kulikuwa vyumba vitatu vya walinzi kila upande wa mulango, vipimo vya miimo yake na nguzo yake vilikuwa kama vile vya mulango wa kwanza. Urefu wote wa ile njia ulikuwa kwa jumla metre makumi mbili na tano na upana wake metre kumi na mbili na nusu. Chumba cha kuingilia na madirisha na nguzo zake, pamoja na ile miti ya ngazi iliyochorwa juu ya ukuta, vyote vilifanana na vile vya mulango wa upande wa mashariki. Kutoka hapo penye njia ya kuingilia ya upande wa kaskazini na kuvuka hicho kiwanja cha ndani moja kwa moja kulikuwa njia ingine ya kuingilia iliyoelekea kwenye kiwanja cha ndani, kama ilivyokuwa upande wa mashariki. Yule mutu alipima urefu wa kutoka kwenye njia mpaka kwenye njia, akapata metre makumi tano. Yule mutu akanipeleka upande wa kusini; huko nako kulikuwa mulango; alipima miimo yake na baraza na vipimo vyake vilikuwa sawa na miimo na baraza zingine. Kulikuwa madirisha pande zote kama ilivyokuwa katika vyumba vingine. Urefu wake ulikuwa metre makumi mbili na tano na upana wake metre kumi na mbili na nusu. Kulikuwa ngazi saba za kupandia kwenye njia hiyo ya kuingilia na kwa mwisho wake kulikuwa baraza iliokuwa inaelekeana na kiwanja. Kulikuwa michoro ya miti ya ngazi kwenye kuta za ndani zilizokuwa mbele ya njia hiyo ya kuingilia. Mbele ya njia hiyo ya kuingilia kulikuwa njia ya kuingilia kwenye kiwanja cha ndani. Yule mutu akapima urefu kati ya hizo njia, akapata metre makumi tano. Yule mutu akanipitisha kwenye njia ya kuingilia upande wa kusini, tukafika kwenye kiwanja cha ndani. Aliipima hiyo njia nayo ilikuwa sawa na zile njia zingine za kuingilia kwenye kuta za inje. Vyumba vya walinzi, baraza, na kuta zake vilikuwa na ukubwa ule ule kama vile vingine; kulikuwa vilevile madirisha kandokando ya hiyo njia ya kuingilia na kwenye baraza. Ilikuwa na urefu metre makumi mbili na tano na upana metre kumi na mbili na nusu. Kulikuwa vyumba kandokando ya hiyo njia ya kuingilia, vikiwa na urefu wa metre makumi mbili na tano na upana wake metre kumi na mbili na nusu. Ile baraza ilikuwa inaelekea kiwanja cha inje. Na kulikuwa michoro ya miti ya ngazi kwenye nguzo kandokando ya hiyo njia ya kuingilia. Kulikuwa ngazi nane za kupandia kwenye mulango huu. Yule mutu alinipeleka upande wa mashariki wa kiwanja cha ndani. Akaipima ile njia ya kuingilia, nayo ilikuwa na urefu kama zile njia zingine za kuingilia. Vyumba vyake vya walinzi, nguzo zake za ndani pamoja na baraza vilikuwa na ukubwa kama vile vingine. Kulikuwa madirisha pande zote hata kwenye baraza na chumba cha kuingilia. Urefu wake ulikuwa metre makumi mbili na tano na upana wake metre kumi na mbili na nusu. Kile chumba cha kuingilia kilikuwa kinaelekea kwenye kiwanja cha inje. Miti ya ngazi ilichorwa kwenye kuta kwenye nafasi ya kupitia. Kulikuwa ngazi nane za kupandia kuelekea kwenye mulango huu. Kisha yule mutu akanipeleka kwenye njia ya kuingilia upande wa kaskazini. Basi, akaipima hiyo njia ya kuingilia, nayo ilikuwa sawa na zile njia zingine. Huko nako kulikuwa vyumba vya walinzi, kuta za ndani zilizopambwa, baraza ya kuingilia na madirisha pande zote. Urefu wake wote ulikuwa metre makumi mbili na tano na upana metre kumi na mbili na nusu. Ile baraza ya kuingilia ilikuwa inaelekea kwenye kiwanja cha inje; kulikuwa miti ya ngazi iliyochorwa kwenye kuta za hiyo nafasi ya kupitia. Kulikuwa vilevile ngazi nane za kupandia kuelekea kwenye mulango huu. Kwenye kiwanja cha inje, kulikuwa chumba cha zaidi kilichounganishwa na njia ya kuingilia ya ndani kwa upande wa kaskazini. Chumba hicho kilikuwa kinaelekea baraza ya kuingilia, na huko walisafishia nyama waliochinjwa kwa ajili ya sadaka za kuteketezwa nzima. Halafu katika baraza karibu na njia kulikuwa meza mbili upande mumoja na zingine mbili upande mwingine. Meza hizo zilitumika kuwa pahali pa kuchinjia sadaka ya kuteketezwa, sadaka ya usamehe wa zambi na sadaka ya malipo ya kosa. Inje ya baraza hiyo, kulikuwa meza mbili upande mumoja na mbili upande mwingine wa njia ya kuingilia kwenye mulango wa kaskazini. Meza zote ambazo zilitumiwa kwa kuchinjia nyama wa sadaka zilikuwa nane: meza ine ndani ya baraza na meza ine inje ya baraza. Kulikuwa vilevile meza ine ndani ya baraza zilizotumiwa kuandalia sadaka za kuteketezwa. Meza hizo zilikuwa zimejengwa kwa mawe yaliyochongwa. Urefu wa kwenda juu wa kila meza ulikuwa sentimetre makumi tano na upande wake wa juu ulikuwa muraba wenye upana wa sentimetre makumi saba na tano pande zote. Vifaa vyote vya kuchinjia sadaka za kuteketezwa na sadaka zingine viliwekwa juu ya meza hizo. Ndani ya baraza hilo kulizungukwa na vijiti vya kutundikia, na nyama ziliwekwa juu ya meza. Inje ya njia ya ndani kulikuwa vyumba vya walinzi kwenye kiwanja cha ndani kilichokuwa upande wa kaskazini wa njia. Vyumba hivyo vilielekea upande wa kusini. Chumba kimoja kilichokuwa upande wa mulango wa mashariki kilielekea upande wa kaskazini. Yule mutu akaniambia hivi: Chumba hiki kinachoelekea upande wa kusini ni kwa ajili ya makuhani wanaotumika katika nyumba ya Yawe, na chumba kinachoelekea upande wa kaskazini ni kwa ajili ya makuhani wanaotumika kwenye mazabahu. Makuhani hawa ni wale wa ukoo wa Zadoki, ndio hao kati ya watu wa kabila la Lawi wanaoruhusiwa kwenda mbele ya Yawe. Yule mutu akapima kiwanja cha ndani, nacho kilikuwa muraba: pande zote zilikuwa na upana wa metre makumi tano. Mazabahu yalikuwa mbele ya nyumba ya Yawe. Kisha, alinipeleka kwenye baraza la kuingilia ndani ya nyumba ya Yawe. Akapima mulango, nao ulikuwa na kimo cha metre mbili na nusu na upana wa metre saba. Na kuta zake zilikuwa na unene metre moja na nusu kila upande. Kulikuwa ngazi za kupandia kwenye baraza la chumba cha kuingilia, ambalo lilikuwa na urefu wa metre kumi na upana metre sita. Kulikuwa nguzo mbili, nguzo moja kila upande wa mulango. Kisha, yule mutu akanipeleka kwenye baraza la ndani, Pahali Patakatifu. Akaipima nafasi iliyoelekea humo ndani, nayo ilikuwa na urefu wa metre tatu, na upana wa metre tano. Nafasi hiyo ilikuwa na kuta kila upande zenye unene wa metre mbili na nusu. Akapima baraza lenyewe, nalo lilikuwa na urefu wa metre makumi mbili na upana metre kumi. Kisha akaenda kwenye chumba cha ndani kabisa. Akaipima nafasi iliyoelekea huko, nayo ilikuwa na kimo cha metre moja na upana metre tatu na nusu. Nafasi hiyo ilikuwa na kuta kila upande zenye unene wa metre tatu na nusu. Akakipima chumba chenyewe, nacho kilikuwa cha muraba pande zake zikiwa na upana wa metre kumi. Chumba hiki kilikuwa mbele ya baraza la katikati. Kisha, akaniambia: Hapa ndipo Pahali Patakatifu Sana. Yule mutu aliupima unene wa ukuta wa nyumba ya Yawe, nao ulikuwa metre tatu. Kulikuwa mufululizo wa vyumba vidogovidogo vilivyozunguka nyumba ya Yawe, vyenye upana wa metre mbili. Vyumba hivi vilikuwa katika majengo ya gorofi tatu, na kila gorofi ilikuwa na vyumba makumi tatu. Ukuta wa inje wa hekalu kila kwenye gorofi ulikuwa mwembamba kuliko ule wa gorofi ya chini, kusudi vile vyumba vikuwe imara bila kuutegemea ukuta wa hekalu. Kwa upande, zile kuta za hekalu zikitazamwa kutokea inje, zilionekana kuwa na unene uleule toka chini mpaka juu. Kuelekea ukuta wa inje wa nyumba ya Yawe, inje ya vyumba, kulikuwa ngazi mbili, ambazo zilifanya ikuwe vyepesi kwenda juu kutokea gorofi ya chini mpaka ile ya juu. Kisha, nikaona kwamba hekalu lilikuwa likizungukwa na sakafu iliyonyanyuliwa, nayo ilikuwa ndio musingi wa zile gorofi tatu mbele ya hekalu, kimo cha musingi wa gorofi hizo ulikuwa sawa na ule ufito wa kupimia, metre tatu. Unene wa ukuta wa inje wa vyumba vya ndani ulikuwa metre mbili na nusu. Nafasi wazi kati ya vyumba vya pembeni mbele ya hekalu na vyumba vya walinzi vilikuwa na upana wa metre kumi, kuzunguka hekalu. Kulikuwa milango kwenye vyumba vya pembeni kutokea kwenye kiwanja, mumoja upande wa kaskazini na mwingine upande wa kusini. Na musingi uliounganishwa na kiwanja ulikuwa na upana wa metre mbili na nusu. Kwa mwisho kabisa wa kiwanja, upande wa magaribi kulikuwa jengo lenye urefu wa metre makumi ine na tano na upana wa metre makumi tatu na tano. Kuta zake zilikuwa na unene wa metre mbili na nusu. Yule mutu akapima upande wa inje wa hekalu nao ulikuwa na urefu wa metre makumi tano. Tokea nyuma ya nyumba ya Yawe kupitia ile nafasi ya kupitia, mpaka mwisho wake, upande wa magaribi, umbali wake ulikuwa vilevile metre makumi tano. Urefu mbele ya hekalu tangu upande huu mpaka upande huu ukichanganya na ile nafasi wazi, ulikuwa vilevile metre makumi tano. Yule mutu akapima urefu wa jengo mpaka magaribi pamoja na mabaraza yake pande zake zote, nalo lilikuwa na urefu wa metre makumi tano. Chumba cha kuingilia katika hekalu, Pahali Patakatifu, na Pahali Patakatifu Sana, vyote vilipambwa kwa mbao tangu kwenye sakafu mpaka kwenye madirisha. Madirisha haya yangeweza kufunikwa. Mpaka kwenye nafasi juu ya mulango hata kwenye chumba cha ndani na inje yake, vilevile juu ya kuta ndani ya chumba cha ndani na kwenye baraza kulikuwa michoro iliyofanana na miti ya gazi na picha za makerubi. Kisha kila muti wa ngazi kulichorwa picha ya kerubi kukizunguka chumba chote. Kila kerubi alikuwa na nyuso mbili: uso wa mwanadamu ulioelekea kwenye muti wa ngazi upande mumoja na uso wa simba ulioelekea kwenye muti wa ngazi upande mwingine. Hivi ndivyo ilivyokuwa kwenye nyumba nzima, tangu sakafu mpaka juu ya milango kulichorwa makerubi na miti ya ngazi. Miimo ya Pahali Patakatifu ilikuwa ya muraba. Mbele ya mulango wa kuingilia Pahali Patakatifu Sana kulikuwa kitu kilichoonekana kama mazabahu ya mbao. Urefu wake kwenda juu ulikuwa metre moja na nusu na upana wa metre moja. Pembe zake, tako lake, na pande zake zote zilikuwa zimetengenezwa kwa mbao. Yule mutu akaniambia hivi: Hii ndiyo meza inayokaa mbele ya Yawe. Kulikuwa mulango wa kuingia kwenye baraza la hekalu na mulango wa kuingia kwenye Pahali Patakatifu Sana. Milango hiyo ilikuwa na sehemu mbilimbili, kwa hiyo kila mulango uliweza kufunguka katikati. Kwenye mulango wa kuingilia kwenye baraza kulichorwa makerubi na miti ya ngazi kama ilivyokuwa kwenye kuta. Na kulikuwa kifuniko cha ubao kikifunika mulango kwa inje kwenye sehemu ya kuingilia ndani. Pembeni ya chumba hiki, kulikuwa madirisha madogo na kuta zilipambwa kwa michoro ya miti ya ngazi. Kisha yule mutu alinipeleka kwenye kiwanja cha inje mpaka kwenye jengo lililokuwa upande wa kaskazini, naye akaniingiza kwenye vyumba vinavyoelekea kiwanja cha hekalu na jengo lililokuwa upande wa kaskazini. Jengo hili lililokuwa upande wa kaskazini lilikuwa na urefu wa metre makumi tano na upana wa metre makumi mbili na tano. Kulikuwa gorofi tatu zilizounganisha metre kumi za kiwanja cha ndani na zikielekea sakafu ya kiwanja cha inje. Upande wa kaskazini wa jengo hilo, kulikuwa njia ya kupitia yenye upana wa metre tano na urefu wake metre makumi tano. Milango yake ilikuwa upande wa kaskazini. Vyumba katika hatua ya juu vilikuwa vyembamba kuliko vile vya katikati na vya chini maana vilikuwa mbali zaidi. Vile vyumba vya juu kabisa vilijengwa kwenye miinuko na havikusaidiwa na nguzo kama majengo mengine kwenye kiwanja cha inje. Kulikuwa ukuta mbele ya vyumba kuelekea kiwanja cha inje ukiwa na urefu wa metre makumi mbili na tano. Wakati vile vyumba kwenye kiwanja cha inje vikiwa na urefu wa metre makumi mbili, vile vinavyoelekea hekalu vilikuwa na urefu wa metre makumi tano. Chini ya vyumba hivi kulikuwa njia ya kupitia tokea upande wa mashariki kwa mwisho wa jengo, ikiwa mutu anaingia tokea kiwanja cha inje ambako ukuta wa inje unaanzia. Kwenye upande wa kusini kulikuwa jengo lingine sawa na lile lingine, si mbali na jengo la upande wa magaribi kwa mwisho wa hekalu. Mbele ya vyumba hivyo kulikuwa njia ya kupitia kama ile ya upande wa kaskazini. Jengo hilo lilikuwa na vipimo vilevile kama vya lile lingine, maingilio, magawanyo na milango ilifanana na ile ingine. Kulikuwa mulango chini ya vyumba kwenye upande wa kusini wa jengo, kwa mwisho wa upande wa mashariki ambako ukuta ulianzia. Yule mutu akaniambia: Vyumba hivi vyote ni vitakatifu. Ndani ya vyumba hivi makuhani wanaoingia mbele ya Yawe, wanakula sadaka takatifu kabisa: sadaka takatifu kabisa na humo ndimo munamowekwa sadaka za vyakula, sadaka za kuomba kusamehewa zambi na sadaka kwa ajili ya malipo ya kosa kwa sababu pahali hapo ni patakatifu. Makuhani ambao watakuwa wakitumika katika Pahali Patakatifu, wanapotaka kwenda kwenye kiwanja cha inje, ni lazima waache humo nguo zao walizovaa walipokuwa wanatumika mbele ya Yawe kwa sababu nguo hizo ni takatifu. Ni lazima wavae nguo zingine mbele ya kutoka inje ambako watu wanakusanyika. Mutu yule alipokwisha kupima eneo la ndani la nyumba ya Yawe, alinitoa inje kupitia mulango wa mashariki na kulipima eneo la inje. Alitwaa ule ufito wake wa kupima na kuupima upande wa mashariki, nao ulikuwa metre mia mbili makumi tano. Akaupima upande wa kaskazini kwa kutumia ufito wake, nao ulikuwa metre mia mbili makumi tano. Kisha akaupima upande wa kusini kwa kutumia ufito wake, nao ulikuwa metre mia mbili makumi tano. Kisha akageuka na kupima upande wa magaribi kwa kutumia ufito wake, nao ulikuwa metre mia mbili makumi tano. Hivyo akakuwa amepima pande zote, nazo zilikuwa metre mia mbili makumi tano kila upande. Ukuta huo ulitenganisha kati ya eneo takatifu na lile la kawaida. Kisha, yule mutu akanipeleka kwenye mulango unaoelekea upande wa mashariki. Utukufu wa Mungu wa Israeli ulitokea upande wa mashariki. Pamoja nao kulikuwa mushindo wa kuja kwake kama mushindo wa maji mengi, inchi ilingaa kwa utukufu wake. Maono hayo yalikuwa kama maono niliyoyaona wakati Mungu alipokuja kuuangamiza Yerusalema. Vilevile yalifanana na maono niliyoyaona karibu na muto Kebari. Nikaanguka uso mpaka chini. Nao utukufu wa Yawe uliingia katika nyumba ya Yawe kwa njia ya mulango wa mashariki. Kisha roho akanitwaa na kunipeleka kwenye kiwanja cha ndani. Nikaona utukufu wa Yawe ukiwa umeijaza nyumba ya Yawe. Yule mutu akiwa anasimama karibu nami, nilisikia mutu fulani akisema nami kutoka katika nyumba ya Yawe; naye akaniambia: Wewe mwanadamu! Hapa ndipo pahali pa kiti changu cha kifalme, pahali ninapoweka miguu yangu. Nitakaa kati ya watu wa Israeli milele. Na Waisraeli hawatalichafua jina langu, wao wenyewe, wala wafalme wao kwa kuziabudu sanamu au kuzika maiti za wafalme wao pahali hapa. Wafalme wao walijenga vizingiti na miimo ya nyumba zao za kifalme karibu na vizingiti vya nguzo za hekalu langu, hivyo kati yangu na wao ulikuwa ni ukuta tu. Walichafua jina langu takatifu kwa machukizo yao waliyotenda, ndiyo maana nimewaangamiza kwa hasira yangu. Sasa waache kuziabudu sanamu na waziondoe maiti za wafalme wao mbali nami, nami nitakaa kati yao milele. Sasa, ewe mwanadamu, uwaelezee Waisraeli habari za nyumba ya Mungu na wajifunze taswira yake. Wapate haya kutokana na machukizo yao waliyotenda. Wakipata haya kutokana na matendo yao, waeleze taswira ya nyumba ya Mungu: taswira yake yenyewe, milango ya kuingilia na kutokea, umbo lake lote, mipango ya kila kitu, kanuni zake na masharti yake. Uwaandikie hayo yote waziwazi kusudi waweze kuona namna yote yalivyopangwa na waweze kuzifuata kanuni na masharti yake. Hii ni sheria juu ya nyumba ya Yawe: Eneo lote linalozunguka nyumba ya Yawe juu ya mulima linapaswa kuwa takatifu kabisa. Vipimo vya mazabahu, vitakuwa vilevile kama vipimo vya hekalu. Kutakuwa musingi wenye urefu wa sentimetre makumi tano na upana wa sentimetre makumi tano kuzunguka musingi wa mazabahu, pamoja na ukingo wenye urefu kuenda juu wa sentimetre makumi mbili na tano. Sehemu ya mazabahu itakayokuwa chini kabisa tokea juu ya musingi itakuwa na kimo cha metre moja. Sehemu itakayofuata itawekwa nyuma kutoka kwenye ukingo sentimetre makumi tano muzunguko, na kimo cha metre mbili. Sehemu itakayofuata nayo itawekwa nyuma ya ukingo sentimetre makumi tano muzunguko. Sehemu hii ya juu, ambayo itatumika kuteketezea sadaka, itakuwa muraba, kila upande metre mbili. Mujengo wa pembe za sehemu hii ya juu zitainuka kuliko sehemu zingine. Sehemu ya juu ya mazabahu itakuwa muraba, metre sita kila upande. Sehemu ya katikati, itakuwa muraba, sentimetre saba kila upande, nayo itakuwa na ukingo pembeni wenye kimo cha sentimetre makumi mbili na tano. Kutakuwa mufereji wenye upana wa sentimetre makumi tano. Na kutakuwa ngazi za kupandia kwenye mazabahu kila upande. Bwana wetu Yawe akaniambia. Wewe mwanadamu! Yawe anasema hivi: Wakati mazabahu itakapojengwa utaitakasa, kwa kutoa sadaka za kuteketezwa juu yake na kuinyunyizia damu ya nyama waliotolewa. Wale makuhani wanaokuwa wa kabila la Lawi ambao ni wazao wa Zadoki, ndio tu watakaokaribia mbele yangu kwa kunitumikia. –Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe.– Utawapa ngombe dume muchanga kuwa sadaka ya kusamehewa zambi. Utatwaa damu yake na kuitia juu ya pembe ine za mazabahu na juu ya chongo ine za daraja na juu ya muzunguko wake pande zote. Hivyo ndivyo utakavyoisafisha mazabahu na kuitakasa. Utatwaa vilevile ngombe dume aliyetolewa kuwa sadaka ya kusamehewa zambi; watamuteketeza katika pahali palipochaguliwa ndani ya nyumba ya Yawe, lakini inje ya Pahali Patakatifu. Kesho yake, utatoa beberu asiyekuwa na kilema, kuwa sadaka ya kusamehewa zambi; mazabahu itatakaswa kama ilivyotakaswa kwa damu ya ngombe dume. Utakapokwisha kuitakasa, utatwaa ngombe dume mudogo asiyekuwa na kilema na kondoo dume mumoja asiyekuwa na kilema na kuwaleta mbele yangu. Makuhani watawapakaa chumvi na kuwatoa kuwa sadaka ya kuteketezwa kwa Yawe. Kwa muda wa siku saba, kila siku utatoa beberu mumoja akuwe sadaka ya kusamehewa zambi. Vilevile watatoa ngombe dume mumoja na kondoo dume mumoja asiyekuwa na kilema. Hivyo kwa muda wa siku saba, utafanya upatanisho na kuisafisha, na hivyo utatakasa mazabahu. Kisha siku hizo saba, tokea siku ya nane na kuendelea, makuhani watatoa sadaka zenu za kuteketezwa na sadaka zenu za amani. Nami nitawakubali. –Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe. Yule mutu akanirudisha kwenye mulango wa inje unaoelekea upande wa mashariki, inje ya pahali patakatifu, nao ulikuwa umefungwa. Yawe akaniambia hivi: Mulango huu utaendelea kufungwa. Hakuna mutu yeyote anayeruhusiwa kuutumia, kwa sababu mimi Yawe, Mungu wa Israeli, nimeingia kupitia mulango ule. Hivyo utadumu ukiwa umefungwa. Hata hivyo, mukubwa anayetawala anaweza kwenda huko na kula chakula chake kitakatifu mbele yangu. Anapaswa kuingia na kutokea kwenye mulango wa chumba cha kuingilia. Yule mutu akanipeleka mbele ya nyumba ya Yawe, kwa njia ya mulango wa kaskazini. Nilipoangalia, nikaona utukufu wa Yawe umeijaza nyumba ya Yawe. Hapo nikaanguka uso mpaka chini. Yawe akaniambia: Wewe mwanadamu! Angalia vizuri mambo yote unayoona na kusikia. Nitakuelezea maagizo yote ya nyumba ya Yawe na sheria zake zote. Shika ndani ya moyo wako kwa uangalifu, ni watu gani wanaoruhusiwa kuingia na kutoka katika nyumba ya Yawe na ni watu gani wamekatazwa kuingia humo. Utawaambia hao watu waasi wa Israeli hivi: Bwana wetu Yawe anasema hivi: Siwezi kuendelea kuyavumilia machukizo yenu yote. Mumelichafua hekalu langu kwa kuruhusu waingie humo watu wasiotahiriwa, watu wasionitii mimi, wakati mafuta na damu vinatolewa kwa ajili yangu. Hivyo, ninyi watu wangu mumelivunja agano langu kwa machukizo yenu yote. Kisha kutimiza kazi ya vitu vyangu vitakatifu, mumeruhusu watu wa mataifa mengine kutimiza kazi hiyo katika hekalu langu. Sasa, Bwana wetu Yawe anasema hivi: Hakuna mutu yeyote wa taifa la kigeni, asiyetahiriwa au asiyenitii mimi atakayeruhusiwa kuingia katika hekalu langu; hata wageni wanaoishi kati ya Waisraeli, hawataruhusiwa. Walawi walioniacha wakati ule Waisraeli walipojitenga nami kwa kufuata miungu yao, watabeba azabu yao. Wataweza tu kutumika katika hekalu langu kama watumishi wakilinda milango ya nyumba yangu, na kutumikia katika nyumba. Wataweza kuchinja nyama wanaotolewa na watu kwa ajili ya kutolewa sadaka za kuteketeza na kuwatumikia watu. Lakini kwa sababu waliongoza ibada za miungu kwa ajili ya watu wa Israeli, wakasukuma watu kutenda zambi, basi, nimeunyoosha mukono wangu kuwaazibu. –Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe.– Nao watabeba azabu yao. Hawatakaribia mbele yangu tena kwa kunitumikia kama makuhani, wala hawatavigusa tena vitu vitakatifu wala vile vitakatifu sana. Lakini watapata haya kwa sababu ya machukizo yao waliyotenda. Hata hivyo, watashika zamu ya kulinda nyumba, wakifanya kazi yote na kazi zote zitakazotendeka humo. Lakini makuhani wa kabila la Lawi ambao ni wazao wa Zadoki walioendelesha kazi yangu katika pahali patakatifu pangu, wakati Waisraeli waliponiacha, hao ndio watakaoendelea kunitumikia na kuja mbele yangu kunitolea mafuta na damu. –Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe.– Hao tu ndio watakaoingia katika hekalu langu, nao watakaribia kwenye mazabahu kwa kunitumikia. Lakini wanapoingia katika kiwanja cha ndani, watavaa nguo za kitani; hawatavaa nguo za sufu watakapotumika katika milango ya kiwanja cha ndani na kwenye nyumba. Watavaa vitambaa vya kitani kwenye vichwa vyao, na makapitula za kitani katika viuno vyao; lakini bila mukaba wowote kwa kuepuka jasho. Watakapotoka kwenda kwenye kiwanja cha inje kwa watu, watatosha nguo walizovaa wakati walipokuwa wanatumika na kuziweka katika vyumba vitakatifu. Ni lazima wavae nguo zingine, kusudi watu wasijitakase kwa kugusa nguo zao. Hawatanyoa vichwa vyao wala kuacha nywele zao zikuwe ndefu. Lakini watapunguza nywele zao. Kuhani yeyote asikunywe divai anapoingia katika kiwanja cha ndani. Kuhani yeyote asioe mwanamuke mujane wala mwanamuke aliyeachana na mume wake. Lakini atamwoa bikira ambaye ni Mwisraeli au mwanamuke aliyefiwa na mume wake aliyekuwa kuhani. Makuhani watafundisha taifa langu kupambanua vitu vinavyokuwa vitakatifu na visivyokuwa vitakatifu, na kuwajulisha tofauti kati ya vitu vinavyokuwa vichafu na visivyokuwa vichafu. Kukikuwa magombano wataamua kadiri ya maamuzi yangu. Katika sikukuu zote watafuata sheria zangu na maamuzi yangu, na kuzitakasa Sabato zangu. Hawatasogelea maiti kusudi wasijichafue. Lakini wataweza kujichafua kwa kusogelea maiti ya baba au mama au mutoto wa kike au wa kiume au dada asiyeolewa. Mumoja wao akijichafua, atakaa na hali hiyo kwa muda wa siku saba. Kisha atakuwa safi. Siku atakapoingia katika patakatifu, katika kiwanja cha ndani kwa kutumika, atatoa sadaka yake ya kusamehewa zambi. –Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe. Makuhani hawatakuwa na haki ya kurizi inchi; haki yao ni kunitumikia mimi. Hamutawapa urizi katika inchi ya Israeli, watakachokuwa nacho ni mimi tu. Watakula sadaka ya vyakula, sadaka ya kusamehewa zambi, na sadaka ya malipo ya kosa. Kila kitu katika Israeli kilichotakaswa kwa Mungu kitakuwa chao. Sehemu ya kwanza ya malimbuko yenu na vya matoleo yenu ya kila aina vitakuwa kwa ajili ya makuhani. Tena mutawapa sehemu ya kwanza ya unga wenu, kusudi mulete baraka juu ya nyumba zenu. Makuhani hawatakula nyamafu au ndege yeyote aliyekufa mwenyewe au aliyeraruliwa na nyama wa pori. Mutakapoigawanya inchi kwa kupiga kura kusudi kila kabila lipate sehemu yake, sehemu moja ya inchi ni lazima itakaswe kwa ajili ya Yawe. Urefu wake utakuwa kilometre kumi na mbili na nusu na upana kilometre kumi. Eneo hilo lote litakuwa takatifu. Ndani yake kutakuwa eneo muraba kwa ajili ya patakatifu, kila upande metre mia mbili makumi tano, na litazungukwa na eneo wazi lenye upana wa metre mia mbili makumi tano. Katika eneo hilo utapima vilevile sehemu yenye urefu wa kilometre kumi na mbili na nusu kwa kilometre tano; humo kutakuwa hekalu langu, Pahali Patakatifu Sana. Eneo hilo litakuwa takatifu katika inchi, na kutengwa kwa ajili ya makuhani wanaomutumikia Yawe katika hekalu lake. Ndani ya eneo hilo kutakuwa nyumba zao na nafasi iliyotakaswa kwa ajili ya hekalu langu. Eneo lingine lenye urefu wa kilometre kumi na mbili na nusu kwa kilometre tano, litatengwa kwa ajili ya miji ya Walawi wanaotumika katika hekalu likuwe urizi wao. Mutapima eneo la muji karibu na eneo takatifu, lenye urefu wa kilometre kumi na mbili na nusu kwa kilometre mbili na nusu. Hilo litakuwa kwa ajili ya mutu yeyote wa Israeli. Mukubwa, naye atapewa eneo lake upande wa mashariki na magaribi wa eneo lililotakaswa kwa ajili ya Yawe. Eneo hilo litaenea tangia upande wa magaribi mpaka kwenye bahari ya Mediteranea na upande wa mashariki mpaka upande wa mashariki wa inchi. Litakuwa na urefu sawa na eneo lililopewa kwa kila kabila la Waisraeli. Huo ndio urizi wa mufalme katika Israeli. Hivyo mufalme hatawatesa watu wangu, lakini ataacha inchi igawanywe kwa Waisraeli kulingana na makabila ya Israeli. Bwana wetu Yawe anasema hivi: Ninyi wakubwa wa Waisraeli, mumefanya zambi vyakutosha. Muache kutesa watu kwa ukali. Muimarishe sheria yangu na haki. Muache kuwafukuza watu wangu katika inchi. –Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe.– Kila mutu anapaswa kutumia mizani na vipimo vya haki. Kwa kipimo cha ulinganifu: efa kwa unga na bati kwa mafuta zina kipimo sawasawa. Hivyo viwili ni sehemu moja ya kumi ya homeri moja. Kwa kupima uzito: gera makumi mbili ni shekeli moja, shekeli makumi tano ni mina moja. Vipimo vya matoleo yenu ya vyakula vitakuwa hivi: sehemu moja ya sita ya efa katika homeri moja ya ngano, na moja ya sita ya efa katika homeri moja ya shayiri. Kiwango cha mafuta kitakuwa hivi: sehemu moja ya bati ya mafuta kutoka kila kori (kori moja ni sawa na homeri moja ambayo ni sawa na bati kumi). Watatoa kondoo mumoja kwa kila kundi la kondoo mia mbili katika jamaa za Waisraeli. Wataleta sadaka za vyakula, sadaka za kuteketezwa kwa moto, na sadaka za amani, kusudi wapate kufanyiwa upatanisho. –Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe.– Watu wote wa inchi watamupatia mufalme wa Waisraeli sadaka hizo. Itakuwa ni mapaswa ya mufalme kuhakikisha kuwa sadaka za kuteketezwa, sadaka za vyakula na sadaka za kinywaji zinazotolewa wakati wa sikukuu ya mwandamo wa mwezi, Sabato, na sikukuu zozote zilizowekwa kwa Waisraeli, zinapatikana. Mufalme yeye mwenyewe atatayarisha sadaka za kusamehewa zambi, sadaka za vyakula, sadaka za kuteketezwa kwa moto, na sadaka za amani kwa kuwafanyia watu wote wa Israeli upatanisho. Bwana wetu Yawe anasema hivi: Siku ya kwanza ya mwezi wa kwanza, mutatoa sadaka ya mwana-ngombe dume asiyekuwa na kilema kwa kutakasa hekalu langu. Kuhani atatwaa sehemu ya damu ya sadaka ya kusamehewa zambi na kuipaka kwenye miimo ya nyumba ya Yawe, pembe za mazabahu, na miimo ya nafasi ya kuingilia kwenye kiwanja cha ndani. Atafanya vile vile siku ya saba ya mwezi huo, kwa ajili ya kila mutu aliyetenda zambi bila kukusudia au kwa kutokujua. Kwa njia hiyo mutaitakasa nyumba ya Yawe. Siku ya kumi na ine ya mwezi wa kwanza, mutafanya sikukuu ya Pasaka. Kwa muda wa siku saba, mutakula mikate isiyotiwa chachu. Siku hiyo, mufalme atatoa ngombe dume mumoja kwa ajili ya sadaka ya kusamehewa zambi kwa ajili yake mwenyewe na kwa ajili ya watu wote wa Israeli. Kila siku, katika muda huo wa siku saba, atamutolea Yawe sadaka ya ngombe dume saba na kondoo dume saba wasiokuwa na kilema kwa kuwateketeza kwa moto. Tena ni lazima atoe sadaka kila siku kuwa sadaka ya kusamehewa zambi. Kisha atatengeneza sadaka ya unga kilo kumi kwa kila ngombe dume na kilo kumi kwa kila kondoo dume, halafu litre tatu za mafuta kwa kila kilo kumi za unga. Katika siku ya kumi na tano ya mwezi wa saba, na kwa muda wa siku saba za sikukuu, mufalme atatoa mahitaji kwa ajili ya sadaka za kusamehewa zambi, sadaka za kuteketezwa kwa moto, sadaka za vyakula na mafuta. Bwana wetu Yawe anasema hivi: Mulango wa kiwanja cha ndani unaoelekea upande wa mashariki utafungwa siku zote sita za kazi. Siku za Sabato na siku za mwandamo wa mwezi utafunguliwa. Tokea inje, mufalme ataingia katika baraza ya ndani kwa kupitia kwenye mulango wa baraza hiyo. Naye atasimama karibu na nguzo ya mulango, wakati makuhani wanateketeza sadaka zake za kuteketezwa kwa moto na sadaka za amani. Kisha mufalme huyo atainama chini kwenye mulango kwa kuabudu na kisha atatoka inje. Mulango utabaki wazi mpaka magaribi. Kila siku ya Sabato na sikukuu ya mwandamo wa mwezi, watu wote wataniabudu mimi Yawe mbele ya mulango. Siku ya Sabato, mufalme ataleta kwa Yawe wana-kondoo sita na kondoo dume mumoja wote wasiokuwa na kilema kama sadaka ya kuteketezwa kwa moto. Pamoja na kila kondoo dume, ataleta sadaka ya unga litre kumi na saba na nusu, lakini pamoja na kila mwana-kondoo ataleta sadaka yoyote anayoweza. Na kwa kila sadaka ya unga, ataleta litre tatu za mafuta. Wakati wa sikukuu ya mwandamo wa mwezi atatoa mwana-ngombe dume, wana-kondoo sita, na kondoo dume mumoja; wote wasiokuwa na kilema. Pamoja na kila ngombe dume na kila kondoo dume anayetolewa sadaka, kunapaswa kuwa litre kumi na saba na nusu za unga, na pamoja na kila mwana-kondoo, kunapaswa kuwa chochote ambacho mufalme anatoa. Tena kwa kila sadaka ya unga, kunapaswa kutolewa litre tatu za unga. Mufalme anapotoka anapaswa kutokea kwa njia ileile aliyoingilia. Watu wanapokuja kumwabudu Yawe wakati wa sikukuu yoyote, wale walioingia kwa njia ya mulango wa kaskazini, watatoka kwa njia ya mulango wa kusini; na wale walioingia kwa mulango wa kusini, watatoka kwa njia ya mulango wa kaskazini. Mutu asirudi kwa njia ya mulango alioingilia, lakini atatoka kwa njia ya mulango unaokuwa mbele yake. Mufalme ataingia ndani watu wanapoingia, na atatoka wanapotoka. Wakati wa siku za sikukuu na siku zilizopangwa, sadaka za unga zitakuwa litre kumi na saba zikiandamana na kila ngombe dume au kondoo dume, na chochote ambacho anayeabudu anaweza kutoa kwa kila mwana-kondoo. Kwa kila sadaka ya unga atatoa litre tatu za mafuta. Mufalme anapotaka kumutolea Yawe sadaka kwa mapenzi yake, ikiwa ni sadaka ya kuteketezwa au sadaka ya amani, watamufungulia mulango wa kiwanja cha ndani unaoelekea upande wa mashariki. Atatoa sadaka kama anavyofanya siku ya Sabato, na anapotoka, mulango ufungwe nyuma yake. Kila siku asubui mutamutolea Yawe mwana-kondoo wa mwaka mumoja asiyekuwa na kilema, ambaye atateketezwa kwa moto. Vilevile kila siku, sadaka ya kilo mbili za unga itatolewa asubui pamoja na litre moja ya mafuta ya muzeituni yakichanganywa na unga. Inafaa kufuata maagizo za sadaka hii kwa Yawe milele. Mwana-kondoo, unga na mafuta vinapaswa kutolewa kila siku asubui kwa Yawe milele. Bwana wetu Yawe anasema hivi: Ikiwa mufalme anamupa mumoja kati ya wana wake zawadi ya sehemu ya inchi, zawadi hiyo itakuwa mali ya huyo kijana milele kama sehemu ya jamaa yake. Lakini ikiwa atamupa mumoja kati ya watumishi wake sehemu yoyote ya inchi yake, zawadi hiyo itakuwa mali yake mpaka mwaka wa kuachwa huru. Kwa hiyo ndipo itamurudilia tena mufalme. Ni yeye tu na watoto wake wa kiume wanaoweza kuirizi kwa siku zote. Mufalme hapaswi kunyanganya hata kidogo mali ya watu. Sehemu ya inchi yoyote anayowapa watoto wake wa kiume inapaswa kutokana na eneo lake mwenyewe. Hivyo hatawatesa watu wangu kwa kuwanyanganya urizi wao. Kisha, yule mutu akanipitisha kwenye nafasi ya kupitia kuingia kwenye vyumba vitakatifu vya makuhani vinavyoelekea upande wa kaskazini, karibu na mulango wa kusini wa kiwanja cha ndani. Akanionyesha nafasi moja, upande wa magaribi wa vyumba, akaniambia hivi: Hapa ndipo makuhani watakapopikia nyama ya sadaka ya malipo ya kosa, sadaka ya kusamehewa zambi, na kupika sadaka za vyakula. Kwa hiyo hawatoki inje ya baraza na chochote, kusudi watu wasijichafue kwa kugusa kitu kitakatifu. Kisha akanipeleka kwenye kiwanja cha inje, akanipitisha karibu na pembe ine za kiwanja; kwa kila pembe kulikuwa kiwanja kidogo, ni kusema, kwa pembe ine za kiwanja kulikuwa viwanja vine vidogo vya urefu wa metre makumi mbili na upana metre kumi na tano. Kulikuwa ukuta kukizunguka kila kiwanja, na mafika mbele ya ukuta. Yule mutu akaniambia: Haya ni mafika ambako watumishi wa nyumba ya Yawe watapikia sadaka watu wanazoleta. Yule mutu akanirudisha kwenye kiingilio cha hekalu. Huko, maji yalikuwa yakitoka chini ya kizingiti cha hekalu kuelekea upande wa mashariki, (kwa maana hekalu lilielekea upande wa mashariki). Maji yalikuwa yakitiririka kutoka chini ya upande wa kusini wa mulango wa hekalu, upande wa kusini wa mazabahu. Kisha akanipeleka inje kwa njia ya mulango wa kaskazini. Akanizungusha kwa njia ya inje mpaka kwenye mulango wa inje, upande wa mashariki; na maji yalikuwa yanatoka upande wa kusini. Yule mutu akapima kwa ufito wake, akapima metre mia tano kwenda chini upande wa mashariki, akanipitisha kwenye maji. Maji yalifika kwenye miguu tu. Kisha akapima tena metre mia tano, akaniongoza kuvuka maji. Maji yakafika mpaka kwa magoti yangu. Akapima tena metre zingine mia tano, naye akaniongoza kuvuka maji. Maji yakafika mpaka kwenye kiuno changu. Akapima metre mia tano zingine, na muto ukakuwa na kilindi kirefu hata sikuweza kuuvuka tena. Haikuwezekana kuuvuka lakini kwa kuogelea. Yule mutu akaniambia: Wewe mwanadamu! Shika mambo hayo yote kwa uangalifu. Kisha, akanirudisha mpaka kwenye ukingo wa muto. Nilipofika huko niliona miti mingi sana kwenye kingo za muto. Akaniambia: Maji haya yanatiririka kupitia katika inchi mpaka katika bonde la Yordani, na yakifika huko yatayafanya maji ya bahari ya Chumvi kuwa maji mazuri. Kila pahali muto huu utakapopita, kutaishi aina zote za nyama na samaki. Muto huu utayafanya maji ya bahari ya Chumvi kuwa maji baridi. Kokote utakakopita utaleta uzima. Wavuvi watasimama kandokando ya bahari, na nafasi toka Engedi mpaka Eni-Eglaimu itakuwa ya kuanikia nyavu. Kutakuwa aina nyingi za samaki kama zinavyokuwa katika bahari ya Mediteranea. Lakini sehemu zake zenye majimaji na tingitingi kandokando ya bahari, zitakuwa na maji mazuri. Lakini hayo yatabaki kuwa maji ya chumvi. Kisha kwa ukingo wa muto huo kutaota kila namna ya miti inayotoa chakula. Majani yake hayatanyauka wala miti hiyo haitaacha kuzaa matunda. Itazaa matunda mapya kila mwezi, kwa sababu inapata maji yanayotiririka kutoka hekalu la Mungu. Matunda yake yatakuwa chakula na majani yake yatatumika kwa kuponyesha magonjwa. Bwana wetu Yawe anasema hivi: Hii ndiyo mipaka ya inchi mutakayoigawanyia makabila kumi na mawili ya Waisraeli. Lakini kabila la Yosefu lipewe mara mbili. Ninyi wote mutagawanyana sawa. Niliapa kuwa nitawapa babu zenu inchi hii, nayo itakuwa mali yenu. Upande wa kaskazini mupaka utapita kutoka bahari ya Mediteranea, kuelekea muji wa Hetiloni, hata pahali pa kuingia Hamati na kuendelea mpaka Zedada. Kutoka hapo utaendelea mpaka Berota na Sibraimu (unaokuwa kati ya Damasiki na Hamati), na mpaka muji wa Hazori-Hatikoni unaokuwa katika inchi ya Haurani. Hivyo mupaka utakwenda kutokea bahari ya Mediteranea kuelekea mashariki mpaka katika muji wa Hazorenoni ukipakana na maeneo ya Damasiki na Hamati kwa upande wa kaskazini. Upande wa mashariki, mupaka utakuwa muto Yordani unaoelekea kati ya Haurani na Damasiki, Gileadi na inchi ya Israeli. Vilevile mupaka utapitia upande wa mashariki wa bahari ya Chumvi mpaka Tamari. Upande wa kusini, toka Tamari mupaka utaendelea mpaka kwenye chemichemi ya Meriba-Kadesi. Kutoka Meriba-Kadesi mupaka utaelekea kusini magaribi mpaka bahari ya Mediteranea ukipitia upande wa mashariki ya inchi ya Misri. Upande wa magaribi, mupaka ni bahari ya Mediteranea na utapanda upande wa kaskazini mpaka pahali pa kuingilia Hamati. Basi, mutagawanya inchi hii kati yenu kulingana na makabila ya Waisraeli. Mutaigawanya kuwa mali yenu. Wageni watakaokaa kati yenu, wale watakaozalia watoto kati yenu, wapewe vilevile sehemu ya inchi munapoigawanya. Hao wanapaswa kutendewa kama wanainchi wa Israeli na wana haki ya kupiga kura kwa kupata sehemu ya inchi pamoja na makabila ya Waisraeli. Kila mugeni anayekaa nanyi atapewa sehemu yake pamoja na watu wa kabila ambamo anaishi. –Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe. Haya ndiyo majina ya makabila na sehemu zao: Kuanzia kwenye mupaka wa kaskazini kwenye barabara ya Hetiloni mpaka kuingia Hamati hata Hazorenoni unaokuwa katika Damasiki na Hamati upande wa kaskazini na kuendelea kutoka mashariki mpaka magaribi. Eneo hilo litakuwa la kabila la Dani. Eneo linalofuatana na la Dani, kutoka mashariki mpaka magaribi litakuwa la Aseri. Kabila la Nafutali, litapata eneo linalopakana na lile la Aseri, kutoka mashariki mpaka magaribi. Kisha eneo la kabila la Nafutali litafuata eneo la kabila la Manase, kutoka mashariki mpaka magaribi. Eneo linalopakana na eneo la Manase kutoka upande wa mashariki mpaka magaribi litakuwa la kabila la Efuraimu. Eneo linalopakana na eneo la Efuraimu kutoka mashariki mpaka magaribi litakuwa la kabila la Rubeni. Eneo linalopakana na eneo la Rubeni kutoka mashariki mpaka magaribi litakuwa la kabila la Yuda. Kisha eneo la kabila la Yuda, utatenga eneo lenye urefu wa kilometre kumi na mbili na upana kama huohuo, kutoka kaskazini mpaka kusini, na urefu huohuo kutoka mashariki mpaka magaribi, sawasawa na eneo la kabila lolote. Hapo katikati ya eneo hilo patakuwa hekalu la Mungu. Eneo utakalotenga kwa ajili ya Yawe litakuwa lenye urefu wa kilometre kumi na mbili na nusu kwa kilometre kumi. Makuhani watakuwa na eneo lao katika eneo hilo. Eneo hilo litakuwa na urefu wa kilometre kumi na mbili na nusu kutoka mashariki mpaka magaribi, na kilometre tano kutoka kaskazini mpaka kusini. Hekalu la Mungu litakuwa katikati ya eneo hilo. Eneo hilo litakuwa kwa ajili ya makuhani wa uzao wa Zadoki, ambao walinitumikia kwa uaminifu na hawakuasi wakati Waisraeli walipoasi kama Walawi walivyofanya. Hilo litakuwa eneo lao takatifu kutoka katika eneo takatifu la inchi, eneo takatifu kabisa, litakalopakana na eneo la Walawi. Nao Walawi, eneo lao litakuwa upande wa kusini wa eneo la makuhani. Eneo hilo litakuwa na urefu wa kilometre kumi na mbili na nusu kutoka mashariki mpaka magaribi, na upana kilometre tano kutokea kaskazini mpaka kusini. Hakuna sehemu yoyote ya eneo hilo itakayouzishwa au kutolewa kwa mutu yeyote, kwa sababu eneo hilo ni takatifu kwa Yawe; nalo ni bora kuliko yote katika inchi. Ile sehemu ya eneo takatifu iliyobaki, yenye urefu wa kilometre kumi na mbili na nusu na upana kilometre mbili na nusu, hilo ni kwa matumizi ya kawaida ya muji: pahali pa kuishi na eneo la mashamba. Katikati yake kutakuwa muji, nao utakuwa wa muraba, kila upande metre elfu mbili mia mbili na makumi tano. Kuuzunguka muji, kutakuwa na eneo wazi lenye upana wa metre mia moja na makumi mbili na tano. Eneo ambalo litabaki kisha kujengwa kwa hekalu, upande wa kusini wa muji, kilometre tano kwa kilometre mbili na nusu upande wa mashariki, na kilometre tano kwa kilometre mbili na nusu upande wa magaribi, litakuwa eneo la walimaji kwa wakaaji wa muji. Watumishi wote katika muji wa kabila lolote la Waisraeli wanaweza kulima katika eneo hilo. Hivyo, eneo lote utakalotenga, ni kusema eneo takatifu pamoja na eneo la muji litakuwa la muraba, kilometre kumi na mbili na nusu kila upande. Eneo linalobaki katika pande zote za eneo takatifu na eneo la muji, ni kusema lile eneo lenye eneo muraba likiwa na kilometre kumi na mbili na nusu kwa kila upande tokea mashariki mpaka magaribi, kuelekea maeneo ya makabila, litakuwa la mufalme. Lile eneo takatifu ambamo hekalu la Mungu litakuwa katikati yake, na eneo la Walawi pamoja na lile eneo la muji, yatakuwa katikati ya eneo la mufalme. Eneo la mufalme litakuwa katika mupaka wa eneo la kabila la Yuda na eneo la kabila la Benjamina. Makabila yaliyobaki yatagawanyiwa maeneo yao hivi: Kabila la Benjamina litapewa eneo kutoka mashariki mpaka magaribi. Eneo linalopakana na eneo la Benjamina kutoka upande wa mashariki kuelekea upande wa magaribi litakuwa la kabila la Simeoni. Eneo linalopakana na kabila la Simeoni kutoka upande wa mashariki kuelekea upande wa magaribi litakuwa eneo la kabila la Isakari. Eneo linalopakana na kabila la Isakari kutoka upande wa mashariki kuelekea upande wa magaribi, litakuwa eneo la kabila la Zebuluni. Eneo linalopakana na kabila la Zebuluni, kutoka mashariki kuelekea magaribi, litakuwa eneo la kabila la Gadi. Eneo linalopakana na kabila la Gadi kuelekea kusini, mupaka utatoka muji wa Tamari mpaka kwenye chemichemi za Meriba-Kadesi na kupitia upande wa mashariki ya Misri mpaka kwenye bahari ya Mediteranea. Hilo ndilo eneo la makabila ya Waisraeli. Humo ndimo watapewa maeneo yao, kila kabila eneo lake. –Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe. Muji Yerusalema utakuwa na ukuta ambao utakuwa na milango hii ya kutokea na kuingilia: Upande wa kaskazini urefu wa ukuta utakuwa metre elfu mbili mia mbili na makumi tano. Upande huo wa kaskazini utakuwa na milango mitatu: mulango wa Rubeni, mulango wa Yuda na mulango wa Lawi. Ukuta wa upande wa mashariki utakuwa na urefu wa metre elfu mbili mia mbili makumi tano. Upande huo utakuwa na milango mitatu: mulango wa Yosefu, mulango wa Benjamina na mulango wa Dani. Ukuta wa upande wa kusini utakuwa na urefu wa metre elfu mbili mia mbili na makumi tano. Upande huo utakuwa na milango mitatu: mulango wa Simeoni, mulango wa Isakari na mulango wa Zebuluni. Ukuta wa upande wa magaribi utakuwa na urefu wa metre elfu mbili mia mbili makumi tano. Upande huo nao utakuwa na milango mitatu: mulango wa Gadi, mulango wa Aseri na mulango wa Nafutali. Jumla ya urefu wa kuta zote ine utakuwa ni metre elfu kenda. Jina la muji kutokea sasa na kuendelea litakuwa: Yawe Yupo Hapa. Katika mwaka wa tatu wa utawala wa mufalme Yoyakimu wa Yuda, mufalme Nebukadneza wa Babeli alikwenda Yerusalema, akauzunguka muji. Bwana akamwacha Yoyakimu atiwe katika mikono ya mufalme Nebukadneza pamoja na sehemu ya vyombo vya nyumba ya Mungu. Basi mufalme Nebukadneza akakamata wafungwa na vyombo akavipeleka katika inchi ya Babeli, akaviweka katika hazina ya nyumba ya miungu yake. Mufalme Nebukadneza akamwamuru Aspenazi, mukubwa wa watumishi wake, amuchagulie kati ya vijana wa Waisraeli wa jamaa ya kifalme na ya watu wenye heshima. Mufalme alitaka vijana wasiokuwa na kilema, wazuri kwa umbo, wenye ujuzi wa kila hekima, wenye akili na maarifa na wanaofaa kwa kutumika katika nyumba ya kifalme. Alitaka vilevile vijana wale wafundishwe kusoma na kuandika luga ya Wakaldea. Mufalme aliagiza vijana wale wapewe chakula bora ambacho yeye mwenyewe alikula na divai ambayo alikunywa. Aliagiza vilevile vijana wale wafundishwe kwa miaka mitatu, kisha wapelekwe kwa mufalme. Kati ya vijana waliochaguliwa kulikuwa Danieli, Hanania, Misaeli na Azaria, wote wa kabila la Yuda. Yule mukubwa wa watumishi akawapa majina mengine; akamwita Danieli kwa jina la Beltesaza, Hanania kwa jina la Sadiraki, Misaeli kwa jina la Mesaki na Azaria kwa jina la Abedenego. Lakini Danieli aliamua kutojichafua kwa kula chakula bora cha mufalme na kunywa divai yake. Kwa hiyo, alimwomba yule mukubwa amuruhusu asikule vitu hivyo na kujichafua. Basi, Mungu akamujalia Danieli kupendelewa na kuhurumiwa na Aspenazi, yule mukubwa. Lakini, mukubwa yule akamwambia Danieli: Ninaogopa kwamba bwana wangu mufalme ambaye ametoa maagizo juu ya chakula na kinywaji unavyopaswa kutumia, ataona kwamba afya yako si nzuri kama ya wenzako wa umri wako. Hivyo maisha yangu yatakuwa katika hatari. Halafu Danieli akamwendea mutumishi aliyewekwa na mukubwa yule kwa kumulinda yeye na wenzake watatu Hanania, Misaeli na Azaria, akamwambia: Tafazali utujaribu, sisi watumishi wako kwa muda wa siku kumi kwa kutupatia mboga za majani na maji. Kisha, utulinganishe sisi na hao vijana wengine wanaokula chakula cha mufalme, halafu utoe uamuzi wako kulingana na jinsi utakavyoona. Mulinzi akakubaliana nao, akawajaribu kwa muda wa siku kumi. Kisha siku hizo kumi, aliwaangalia akaona kwamba wale vijana waliokula mboga za majani walionekana wenye afya na nguvu kuliko wale wengine wote waliokulishwa chakula cha kifalme. Basi, yule mulinzi akawaacha waendelee kula mboga za majani pahali pa chakula na divai walioamuriwa. Mungu aliwajalia vijana wale wane maarifa na ujuzi katika elimu na hekima. Zaidi ya hayo, alimujalia Danieli ufahamu wa kufasiria maono na ndoto. Muda ulipotimia ambapo wale vijana wangepelekwa kwa mufalme kama alivyokuwa ameagiza, yule mukubwa akawapeleka vijana wote mbele ya Nebukadneza. Mufalme alipozungumuza nao wote, hakuna walioonekana kuwa bora kama Danieli, Hanania, Misaeli na Azaria. Basi, wakakubaliwa kumutumikia mufalme. Jambo lolote la hekima au la maarifa ambalo mufalme aliwauliza alijionea mwenyewe kwamba vijana wale wane walikuwa bora mara kumi kuliko waaguzi na wachawi wote katika utawala wake. Danieli alidumu katika kazi ya nyumba ya mufalme mpaka mwaka wa kwanza wa utawala wa mufalme Kiro. Katika mwaka wa pili wa utawala wake, mufalme Nebukadneza aliota ndoto. Na kwa hiyo roho yake ikahuzunika sana hata hakuweza kupata usingizi. Basi, mufalme akaamuru waganga, walozi na wachawi wa Wakaldea waletwe kusudi wamufasirie ndoto yake. Wote wakakuja na kusimama mbele yake. Mufalme Nebukadneza akawaambia: Niliota ndoto, nayo inanipa wasiwasi, nami ninataka nijulishwe maana yake. Wale Wakaldea wakamwambia mufalme katika luga ya Kiaramu: Uishi milele, ee mufalme! Utuelezee ndoto yako nasi watumishi wako tutakufasiria maana yake. Mufalme akawaambia: Nimetoa neno langu kamili: ikiwa hamutanijulisha ndoto yenyewe na maana yake, mutakatwa vipandevipande na nyumba zenu zitabomolewa. Lakini mukiniambia hiyo ndoto na maana yake, nitawapa zawadi, mapato na heshima kubwa. Basi, munijulishe ndoto hiyo na maana yake! Wao wakamujibu mara ya pili: Mufalme, utuelezee ndoto hiyo, nasi watumishi wako tutakufasiria maana yake. Halafu mufalme akawajibu akisema: Ninajua kweli kwamba munajaribu kupoteza wakati kwa maana munaona kwamba nilikwisha toa neno langu kamili, kwamba musiponijulisha ndoto hiyo, azabu yenu ni moja. Mumepatana kunidanganyadanganya na kuniambia uongo kwa kungojea hali ibadilike. Muniambie ndoto hiyo, nami nitajua kwamba munaweza kunijulisha maana yake. Wale Wakaldea wakamujibu: Mufalme, hakuna mutu yeyote katika dunia anayeweza kutimiza mapenzi yako. Hakuna mufalme yeyote, hata akuwe mukubwa na mwenye nguvu yapata gani aliyepata kuwauliza waganga au walozi au Wakaldea jambo kama hilo. Jambo unalouliza, ee mufalme, ni gumu. Hakuna mutu anayeweza kukufunulia isipokuwa miungu peke yake ambayo haikai kati ya wanadamu. Kusikia hivyo, mufalme Nebukadneza alikasirika na kuwa na hasira sana, akaamuru wenye hekima wote wa Babeli waangamizwe. Basi, tangazo likaenea kuwa wenye hekima wote wauawe; Danieli na wenzake, nao vilevile wakatafutwa kusudi wauawe. Lakini, Danieli akasema na Arioki kwa uangalifu na hekima. Arioki alikuwa ni mukubwa wa waaskari walinzi wa mufalme ambaye alipewa amri ya kuwaua wenye hekima wa Babeli. Danieli akamwuliza: Kwa nini amri ya mufalme ni kali hivyo? Arioki akamwelezea Danieli maneno yote. Halafu Danieli alimwendea mufalme na kumwomba amupatie muda kusudi apate kumujulisha mufalme maana ya ndoto yake. Kisha, Danieli akarudi kwa nyumba, akawajulisha wenzake Hanania, Misaeli na Azaria jambo hilo. Aliwaambia wamwombe Mungu wa mbinguni awaonee huruma juu ya fumbo hilo, kusudi wao wasiangamie pamoja na wenye hekima wengine wa Babeli. Halafu Danieli akafunuliwa fumbo hilo usiku katika maono. Naye Danieli akamushukuru Mungu wa mbinguni, akasema: Jina la Mungu litukuzwe milele na milele. Hekima na nguvu ni vyake. Anabadilisha nyakati na wakati, anaondoa na kuwatawalisha wafalme. Anawapa hekima wenye hekima, anawaongezea wenye maarifa ufahamu. Anafunua siri na mafumbo, anajua kinachokuwa katika giza, mwangaza unakaa kwake. Kwako, ee Mungu wa babu zangu, ninatoa shukrani na kukusifu, maana umenipa hekima na nguvu, umetujulisha kile tulichokuomba, umetujulisha yale maneno ya mufalme. Basi, Danieli akamwendea Arioki aliyekuwa amechaguliwa kuwaangamiza wenye hekima wa Babeli, akamwambia: Usiwaue wenye hekima wa Babeli, lakini unipeleke mimi mbele ya mufalme, nami nitamweleza maana ya ndoto yake. Basi, Arioki akamupeleka Danieli mbele ya mufalme kwa haraka na kumwambia: Nimemupata mutu fulani kati ya wafungwa wa Yuda anayeweza kukufasiria maana ya ndoto yako, ee mufalme. Mufalme akamwuliza Danieli, ambaye vilevile aliitwa Beltesaza: Unaweza kunijulisha ndoto niliyoota na maana yake? Danieli akamujibu mufalme: Hakuna wenye hekima, wachawi, waganga wala waaguzi wanaoweza kukujulisha fumbo hilo lako. Lakini, kuna Mungu mbinguni ambaye anafumbua mafumbo, naye amekujulisha, ee mufalme Nebukadneza, mambo yatakayotukia katika siku zinazokuja. Ndoto yako na maono yaliyokufikia ulipokuwa unalala ni haya: Ee mufalme, ulipokuwa unalala katika kitanda chako, mawazo yalikufikia juu ya mambo yatakayotukia kisha; naye Mungu anayefumbua mafumbo, alikuonyesha yale yatakayotukia. Lakini mimi sikufumbuliwa fumbo hili kwa sababu nina hekima kuliko wanadamu wengine, lakini kusudi wewe mufalme, upate kujulishwa maana ya ndoto yako na kujua mawazo yako. Katika ndoto yako, ee mufalme, uliona sanamu kubwa, yenye nguvu na iliyoangaa sana, ikisimama mbele yako. Sanamu hiyo ilikuwa ya kutisha sana. Kichwa cha sanamu hiyo kilikuwa cha zahabu safi, kifua chake na mikono yake vilikuwa vya feza na tumbo lake na mapaja yake vilikuwa vya shaba. Miguu yake ilikuwa ya chuma na vikanyagio vyake vilikuwa vya muchanganyiko wa chuma na udongo wa mufinyanzi. Ulipokuwa ukiangalia, jiwe liliongoka lenyewe, bila kuguswa, na kuipondaponda miguu ya shaba na udongo wa mufinyanzi ya ile sanamu, na kuivunja vipandevipande. Mara moja chuma, udongo wa mufinyanzi, shaba, feza na zahabu, vyote vikavunjika vipandevipande na vikakuwa kama maganda kwenye nafasi ya kupepetea ngano wakati wa jua. Upepo ukavipeperushia mbali wala hakukubakia hata kipande kimoja. Lakini lile jiwe lililoivunja ile sanamu likageuka kuwa mulima mukubwa na kuijaza dunia yote. Hiyo ndiyo ndoto yako, ee mufalme. Na sasa tutakupa maana yake. Wewe, ee mufalme, mufalme wa wafalme! Mungu amekupa ufalme, uwezo, nguvu na utukufu! Amekupa mamlaka juu ya wanadamu wote, nyama wa pori na ndege wote, popote kule wanapokuwa. Wewe ndiwe kile kichwa cha zahabu! Nyuma yako kutafuata ufalme mwingine, lakini ufalme huo utakuwa zaifu. Huu utafuatwa na ufalme wa tatu unaofananishwa na shaba; huo utaitawala dunia yote. Nyuma ya falme hizo, kutafuata ufalme mwingine wenye kuwa imara kama chuma. Na kama vile chuma kinavyovunja na kupondaponda vitu vyote, ndivyo ufalme huo utakavyovunjavunja na kusaga kabisa falme zilizotangulia. Uliona vilevile kwamba vikanyagio na vidole vya sanamu hiyo vilikuwa nusu udongo wa mufinyanzi na nusu chuma. Hii ina maana kwamba ufalme huo utagawanyika; lakini ndani yake kutakuwa nguvu za chuma kwa sababu kulikuwa chuma kilichochanganyikana na udongo wa mufinyanzi. Kama ulivyoona, vidole vyake vya miguu vilikuwa nusu chuma na nusu udongo wa mufinyanzi, na hii ina maana kwamba ufalme ule utakuwa na sehemu moja yenye nguvu na sehemu ingine yenye uzaifu. Hii ina maana kwamba watawala wa ufalme huo watachanganyikana kwa kuoana na watu wasiokuwa wa taifa lao, lakini hawatafikia kuchanganyikana kama vile chuma kisivyoweza kuchanganyikana na udongo wa mufinyanzi. Wakati wa wafalme wale, Mungu wa mbinguni ataanzisha ufalme ambao hautaangamizwa hata kidogo. Watu wengine hawataushinda na kuutawala ufalme huo, lakini ufalme huo utaziponda na kuzikomesha falme zilizotangulia, nao utadumu milele. Uliliona jiwe lililoongoka lenyewe toka kwenye mulima, bila kuguswa, na jinsi lilivyoivunja vipandevipande ile sanamu iliyotengenezwa kwa chuma, shaba, udongo wa mufinyanzi, feza na zahabu. Ee mufalme, Mungu Mukubwa amekufunulia mambo yatakayotukia nyuma. Ni mimi ninayekuelezea hivyo. Ndoto yako ni ya kweli na maana yake ni ya kuaminiwa. Halafu mufalme Nebukadneza akaanguka uso mpaka chini na kumutukuza Danieli na kuamuru wamutolee Danieli sadaka na ubani. Mufalme akamwambia Danieli: Hakika, Mungu wako ni Mungu wa miungu na Bwana wa wafalme, na ndiye anayefumbua mafumbo kwa sababu ameweza kunifumbulia fumbo hili. Kisha mufalme Nebukadneza akamupandishia Danieli heshima kubwa, akamupa zawadi nyingi kubwakubwa, na kumufanya kuwa mutawala wa jimbo lote la Babeli, na mukubwa wa wenye hekima wote wa Babeli. Danieli akamwomba mufalme, naye mufalme akawaweka Sadiraki, Mesaki na Abedenego kuwa wasimamizi wa mambo ya utawala ya jimbo la Babeli. Lakini Danieli akabakia katika nyumba ya mufalme. Mufalme Nebukadneza alitengeneza sanamu ya zahabu, yenye urefu wa metre makumi mbili na nane na upana wa metre tatu. Akaisimamisha katika bonde la Dura katika jimbo la Babeli. Kisha mufalme akaamuru maliwali, wasimamizi, watawala, washauri, walinzi wa mali, waamuzi, wana sheria na wakubwa wote wa majimbo wahuzurie sikukuu ya kuzindua sanamu aliyosimamisha. Basi, maliwali, wasimamizi, watawala, washauri, walinzi wa hazina, wana sheria na wakubwa wote wa majimbo wakakusanyika tayari kwa muzinduo wa sanamu mufalme Nebukadneza aliyosimamisha. Mutangazaji wa habari akatangaza kwa sauti kubwa: Enyi watu wa makabila yote, mataifa yote na luga zote, munaamuriwa kwamba mukisikia sauti ya baragumu, filimbi, kinubi, zeze, santuri, zomari na sauti za ala nyingine za muziki, munapaswa kuinama chini na kuabudu sanamu ya zahabu mufalme Nebukadneza aliyosimamisha. Na yeyote ambaye hatainama chini na kuiabudu, atatupwa mara moja katika furu la moto mukali. Kwa hiyo, watu wote, mara tu waliposikia sauti za baragumu, filimbi, kinubi, zeze, santuri, zomari na sauti za ala nyingine za muziki, walianguka uso mpaka chini na kuiabudu ile sanamu ya zahabu ambayo mufalme Nebukadneza alisimamisha. Wakati huo, watu wamoja kati ya Wakaldea wakajitokeza na kuwashitaki Wayuda. Walimwambia mufalme Nebukadneza: Uishi milele, ee mufalme! Wewe, ee mufalme, ulitoa amri kwamba kila mutu anaposikia sauti ya baragumu, filimbi, kinubi, zeze, santuri, zomari na kila aina ya muziki, ainame chini na kuiabudu ile sanamu ya zahabu. Na kwamba mutu yeyote asiyeinama chini na kuiabudu sanamu hiyo, atupwe ndani ya furu la moto mukali. Sasa, kuna Wayuda fulani uliowachagua kwa kushugulikia mambo ya utawala wa jimbo la Babeli, nao ni: Sadiraki, Mesaki na Abedenego; watu hawa, ee mufalme, hawakutii amri yako. Wanakataa kuitumikia miungu yako na kuiabudu ile sanamu ya zahabu uliyoisimamisha. Halafu mufalme Nebukadneza, akakasirika, akaamuru Sadiraki, Mesaki na Abedenego waletwe mbele yake. Nao wakawaleta mbele ya mufalme. Mufalme Nebukadneza akawauliza: Ni kweli kwamba wewe Sadiraki, wewe Mesaki na wewe Abedenego, hamwitumikii miungu yangu wala kuiabudu ile sanamu ya zahabu niliyoisimamisha? Basi, mutakaposikia tena sauti ya baragumu, filimbi, kinubi, zeze, santuri, zomari na sauti za ala nyingine za muziki, muko tayari kuinama chini na kuiabudu sanamu niliyotengeneza? Kama mukikataa, mutatupwa mara moja katika furu la moto mukali. Ni mungu gani anayeweza kuwaokoa katika mikono yangu? Sadiraki, Mesaki na Abedenego wakamujibu mufalme: Ee Nebukadneza, sisi hatuhitaji kukujibu juu ya jambo hilo. Mungu wetu ambaye tunamutumikia anaweza kutuokoa. Atatuokoa kutoka furu la moto mukali na vilevile kutoka katika mikono yako, ee mufalme. Lakini, hata kama haitafanyika hivyo, ujue wazi, ee mufalme, kwamba sisi hatutaitumikia miungu yako wala kuiabudu sanamu ya zahabu uliyosimamisha. Kwa hiyo, mufalme Nebukadneza akawaka hasira, sura yake ikabadilika kwa chuki juu ya Sadiraki, Mesaki na Abedenego. Akaamuru kwamba moto wa furu uongezwe mara saba kuliko kawaida yake. Akaamuru watu fulani wenye nguvu kabisa kati ya waaskari wake wawafunge Sadiraki, Mesaki na Abedenego na kuwatupa katika ile furu ya moto mukali. Basi, vijana hao wakafungwa wakiwa wamevaa makoti yao, kanzu zao, kofia na nguo zao zingine, wakatupwa katikati ya ile furu la moto mukali. Kwa vile amri ya mufalme ilikuwa kali, ule moto ulikuwa umewashwa na kuwa mukali sana, hata ndimi za moto zikawateketeza wale watu waliowapeleka Sadiraki, Mesaki na Abedenego. Halafu Sadiraki, Mesaki na Abedenego, wakiwa wamefungwa, wakatumbukia katika ile furu ya moto mukali. Basi, mufalme Nebukadneza akashangaa, akasimama kwa haraka na kuwauliza washauri wake: Si tuliwafunga watu watatu na kuwatupa katika moto? Nao wakamujibu mufalme: Kweli, mufalme! Ndivyo! Kisha akauliza: Lakini sasa mbona ninaona watu wane wakitembeatembea mule ndani ya moto bila kufungwa na wala hawaunguwi, na mutu wa ine anaonekana kama mwana wa miungu? Basi, mufalme Nebukadneza akaukaribia mulango wa furu la moto mukali, akaita: Sadiraki, Mesaki na Abedenego, watumishi wa Mungu Mukubwa, mutoke mukuje hapa! Sadiraki, Mesaki na Abedenego wakatoka ndani ya moto. Maliwali, wasimamizi, wakubwa wa majimbo na washauri wa mufalme, wote wakakusanyika pamoja, wakaona kwamba ule moto haukuweza kuwaunguza hao watatu. Nywele zao hazikuungua, nguo zao hazikuungua wala hawakuwa na harufu yoyote ya moto. Basi, mufalme Nebukadneza akasema: Asifiwe Mungu wa Sadiraki, Mesaki na Abedenego kwa sababu alimutuma malaika wake na kuwaokoa watumishi wake ambao wanamutegemea. Wao walikataa kutii amri yangu ya kifalme, wakaitoa miili yao kama sadaka pahali pa kuabudu mungu mwingine, lakini Mungu wao peke yake. Kwa hiyo, ninaamuru kwamba watu wa kabila lolote, taifa lolote au luga yoyote, watakaosema kitu chochote cha kumuzarau Mungu wa Sadiraki, Mesaki na Abedenego, watakatwa vipandevipande na nyumba zao zitabomolewa. Maana hakuna mungu mwingine anayeweza kuokoa namna hii. Basi, mufalme Nebukadneza akawapandishia vyeo Sadiraki, Mesaki na Abedenego katika jimbo la Babeli. Mufalme Nebukadneza aliwaandikia hivi watu wa makabila yote, mataifa yote na luga zote katika dunia: Ninawatakia amani tele! Nimeona vema kuwajulisha kitambulisho na maajabu ambayo Mungu Mukubwa amenionyesha. Kweli vitambulisho vya Mungu ni kubwa! Maajabu yake ni makubwa sana! Ufalme wake ni ufalme wa milele; ufalme wake unadumu kwa vizazi vyote. Mimi, Nebukadneza, nilikuwa ninaishi katika raha na amani katika nyumba yangu ya kifalme. Lakini nikaota ndoto iliyonitisha; nikiwa nimelala katika kitanda, mawazo na maono yaliniogopesha. Hivyo, nikaamuru wenye hekima wote wa Babeli waletwe mbele yangu kusudi wanielezee maana ya ndoto hiyo. Halafu waganga, walozi, Wakaldea na wenye hekima wakaletwa. Nikawaelezea ndoto yangu, lakini hawakuweza kunieleza maana yake. Kisha, Danieli akafika, anayeitwa vilevile Beltesaza, jina la mungu wangu, ambaye roho ya miungu mitakatifu iko ndani yake, nami nikamwelezea ndoto yangu, nikasema: Ee Beltesaza, unayekuwa mukubwa wa waganga, ninafahamu kuwa roho ya miungu mitakatifu iko ndani yako, na kwamba hakuna fumbo linalokuwa gumu kwako. Hii ndiyo ndoto yangu; uniambie maana yake. Nilipokuwa ninalala, niliona maono haya: Niliona muti murefu sana katikati ya dunia. Muti uliendelea kukomaa, ukakuwa imara na kilele chake kikafika mbinguni. Uliweza kuonekana kutoka kila pahali katika dunia. Majani yake yalikuwa mazuri. Ulikuwa umejaa matunda mengi yaliyotoshelea kwa kulisha dunia nzima. Nyama wote wa pori walipata kivuli chini yake, na ndege wa anga walikaa katika matawi yake. Viumbe vyote vilipata chakula kutoka muti huo. Nilipokuwa ninalala katika kitanda, niliona maono: Mulinzi mutakatifu alishuka kutoka mbinguni. Akalalamika kwa sauti akisema: Mukate muti huu na kuyakatakata matawi yake. Muangushe majani yake na kuyatawanya matunda yake. Nyama wakimbie toka chini yake na ndege kutoka matawi yake. Lakini muache kisiki chake na mizizi yake ndani ya udongo, kwenye majani mabichi ndani ya shamba kikiwa kimefungwa pale kwa munyororo wa chuma na shaba. Muache kilowanishwe na umande wa mbinguni; muache kiishi pamoja na nyama wa pori na kula majani katika mbuga. Akili yake ya kimutu ibadilishwe, akuwe na akili ya nyama kwa miaka saba. Hii ni hukumu iliyotangazwa na walinzi; ni uamuzi wa wanaokuwa watakatifu, kusudi wanadamu wote kila pahali wapate kutambua kwamba Mungu Mukubwa ana mamlaka juu ya falme zote za wanadamu; yeye anamupatia ufalme mutu yeyote anayemupenda, anamufanya kuwa mufalme hata mutu muzaifu wa mwisho. Hii ndiyo ndoto niliyoota mimi Nebukadneza. Sasa, wewe Beltesaza, unielezee maana yake; maana wenye hekima wote katika ufalme wangu hawawezi kuniambia maana yake; lakini wewe utaweza kwa maana roho ya miungu mitakatifu iko ndani yako. Basi, Danieli, aliyeitwa vilevile Beltesaza, akashangaa kwa muda, na mafikiri yake yakamufazaisha. Mufalme akamwambia: Beltesaza, ndoto hii, wala maana yake visikufazaishe! Beltesaza akamujibu: Bwana wangu, ingelikuwa heri ndoto hii na maana yake iwaelekee waadui zako! Muti uliouona ukiwa mukubwa na wenye nguvu, ambao matawi yake marefu yalifika mbinguni, nao ukionekana kutoka kila pahali katika dunia, majani yake yakiwa mazuri, na matunda yake mengi ya kukulisha viumbe vyote, nyama wa pori wakipata kivuli chini yake, na ndege wakikaa katika matawi yake, basi, ni wewe, ee mufalme, ambaye umekuwa mukubwa na mwenye nguvu. Ukubwa wako umefika mpaka mbinguni, na ufalme wako umeenea mpaka miisho ya dunia. Kisha ukaona tena, ee mufalme, Mulinzi mutakatifu akishuka kutoka mbinguni, akaamuru: Mukate muti huu, muuangamize. Lakini muache kisiki chake na mizizi yake katika udongo kwenye majani mabichi ya mashamba, kikiwa kimefungwa pale kwa munyororo wa chuma na shaba. Muache kilowanishwe na umande wa mbinguni; muache kiishi pamoja na nyama wa pori kwa miaka saba. Hii basi, bwana wangu, ndiyo maana ya ndoto yako, kadiri ya uamuzi wa Mungu Mukubwa juu yako: Wewe utafukuzwa mbali na wanadamu. Utaishi pamoja na nyama wa pori, utakula majani kama ngombe; utalowana na umande wa mbinguni. Utakaa katika hali hiyo kwa miaka saba, na kwa mwisho utatambua kwamba Mungu Mukubwa ndiye anayetawala juu ya ufalme wa wanadamu naye anamupa ufalme ule mutu yeyote anayemutaka. Tena amri ile ya kukiacha kisiki na mizizi ya muti huo katika udongo ina maana hii: Wewe utarudishiwa tena ufalme wako wakati utakapotambua kwamba Mungu wa mbinguni ndiye anayetawala. Kwa sababu hiyo, ee mufalme, sikiliza shauri langu. Achana na zambi zako na maovu yako, utende haki na kuwaonea huruma walioteswa; labda muda wako wa kufanikiwa utarefushwa! Hayo yote yalimupata mufalme Nebukadneza. Nyuma ya miezi kumi na miwili, mufalme Nebukadneza alikuwa anatembea juu ya dari ya nyumba ya kifalme katika muji wa Babeli. Basi, akasema kwa sauti: Angalia Babeli, muji mukubwa nilioujenga kwa nguvu zangu ukuwe makao yangu ya kifalme na kwa ajili ya utukufu wangu! Alipokuwa angali anasema maneno hayo, sauti kutoka mbinguni ikamwambia: Ewe mufalme Nebukadneza, sikiliza ujumbe huu juu yako! Umenyanganywa ufalme! Utafukuzwa mbali na wanadamu! Utaishi pamoja na nyama wa pori, na utakula majani kama ngombe! Utakaa katika hali hiyo kwa miaka saba, na kwa mwisho utatambua kwamba Mungu Mukubwa ndiye mwenye uwezo juu ya falme za wanadamu, na anamupa ufalme mutu yeyote anayemutaka. Mara moja jambo hilo juu ya mufalme Nebukadneza likatimizwa. Alifukuzwa mbali na wanadamu, akakuwa anakula majani kama ngombe. Alilowanishwa na umande wa mbinguni, na nywele zake zikakuwa ndefu kama manyoya ya tai, na kucha zake kama za ndege. Kwa mwisho wa ile miaka saba, mimi Nebukadneza niliinua macho yangu kuangalia juu mbinguni na akili zangu zikanirudilia. Nilimushukuru Mungu Mukubwa na kumuheshimu yeye anayeishi milele: Kwa sababu mamlaka yake ni mamlaka ya milele, ufalme wake unadumu kwa vizazi vyote. Wakaaji wote wa dunia si kitu; anafanya anavyotaka na viumbe vya mbinguni, na wakaaji wa dunia; hakuna anayeweza kumupinga, au kusema: Unafanya nini? Wakati uleule akili zangu zikanirudilia; nilirudishiwa vilevile heshima yangu, mamlaka yangu na utukufu wa ufalme wangu. Washauri na wakubwa wangu walikuja kunitafuta, nikarudishwa katika ufalme wangu na kupata heshima kama pale mbele. Na sasa, mimi Nebukadneza ninamusifu na kumutukuza na kumuheshimu Mufalme wa mbinguni. Maana matendo yake yote ni ya haki, naye anawashusha wenye kiburi. Siku moja mufalme Belsasari alifanya karamu kubwa kwa ajili ya maelfu ya wakubwa wake na kunywa divai pamoja nao. Kutokana na kunywa divai, mufalme Belsasari akatoa amri kwamba vile vyombo vya zahabu na feza ambavyo baba yake mufalme Nebukadneza alivyokamata kutoka hekalu la Yerusalema, viletwe kusudi avitumie kwa kunywea divai pamoja na wakubwa wake, wanawake wake na wahabara wake. Basi, vile vyombo vya zahabu na feza vilivyokamatwa katika hekalu kule Yerusalema vikaletwa. Mufalme, wakubwa wake, wanawake wake na wahabara wake wakavitumia kwa kunywea. Walikunywa na kusifu sanamu za miungu iliyotengenezwa na zahabu, feza, shaba, chuma, miti na mawe. Saa ileile, vidole vya mukono wa mwanadamu vikatokea na kuandika kwenye lipu ya ukuta wa nyumba ya kifalme uliopakaliwa chokaa pahali palipoangaziwa vizuri, mbele ya kinara cha taa. Mufalme aliuona mukono ule ukiandika. Basi, mufalme akabadilika rangi na kufazaika kwa ajili ya mawazo yaliyomufikia, viungo vyake vikaregea na magoti yakaanza kutetemeka. Mufalme Belsasari akaamuru kwa sauti kwamba wachawi, Wakaldea wenye hekima na waaguzi waletwe. Walipoletwa, mufalme akawaambia wenye hekima hao wa Babeli: Yeyote atakayesoma maandiko haya na kunijulisha maana yake, atavalishwa nguo nzuri nyekundu za kifalme na mukufu wa zahabu katika shingo lake, na kupewa nafasi ya tatu katika ufalme. Basi, wenye hekima wote wa mufalme wakakuja, lakini hawakuweza kuyasoma maandiko hayo wala kumujulisha mufalme maana yake. Basi, mufalme Belsasari akazidi kuhangaika na rangi yake ikazidi kugeuka, nao wakubwa wake wakakuwa na wasiwasi. Kutokana na kelele za mufalme na wakubwa wake, mama ya mufalme aliingia ndani ya chumba cha karamu, akasema: Uishi milele, ee mufalme! Si lazima mawazo yako yakufazaishe na rangi yako kubadilika. Katika ufalme wako kuna mutu ambaye roho ya miungu mitakatifu iko ndani yake. Wakati wa utawala wa baba yako, mutu huyu alionekana kuwa mwenye ujuzi, ufahamu na hekima kama ya miungu. Baba yako, mufalme Nebukadneza, alimufanya kuwa mukubwa wa waaguzi, wachawi, Wakaldea wenye hekima, na waganga, kwa sababu ana roho njema, maarifa, ujuzi wa kufasiria ndoto, kufumbua mafumbo na kutatua matatizo. Jina la mutu huyo ni Danieli ambaye baba yako alimwita Beltesaza. Basi wamwite, naye atakuelezea maana ya maandiko haya. Basi, Danieli akaletwa mbele ya mufalme, naye mufalme akamwuliza: Wewe ndiwe Danieli, mumoja wa wafungwa ambao baba yangu mufalme, aliowaleta kutoka inchi ya Yuda? Nimesikia kwamba roho ya miungu mitakatifu iko ndani yako, na kwamba una ujuzi, na akili, na hekima ya ajabu. Wenye hekima na wachawi walipoletwa hapa kusoma na kunielezea maana ya maandiko haya, walishindwa. Lakini, nimesikia kwamba wewe unaweza kueleza vitendawili na kutambua mafumbo. Basi, kama ukiweza kusoma maandiko haya na kunielezea maana yake, utavalishwa nguo nzuri ya rangi nyekundu na kuvalishwa mukufu wa zahabu katika shingo lako. Utapewa nafasi ya tatu katika ufalme huu. Danieli akamujibu mufalme Belsasari: Unaweza kubakia na zawadi zako, ee mufalme, au kumupa mutu mwingine. Hata hivyo, ee mufalme, nitakusomea maandiko hayo na kukuelezea maana yake. Ee mufalme, Mungu Mukubwa alimupa baba yako mufalme Nebukadneza ufalme, ukubwa, mamlaka na utukufu. Kwa sababu ya ukubwa aliomupa, watu wa makabila yote, mataifa yote na luga zote walitetemeka na kumwogopa. Nebukadneza aliweza kumwua mutu yeyote aliyetaka na kumwacha muzima mutu yeyote aliyetaka. Aliyetaka kumupandisha cheo alimupandisha, aliyetaka kumushusha cheo alimushusha. Lakini alipoanza kuwa na kiburi, akakuwa na roho ngumu na mwenye majivuno, aliondolewa katika kiti chake cha kifalme, akanyanganywa utukufu wake. Alifukuzwa mbali na wanadamu, akili yake ikafanywa kama ya nyama, akaishi na punda wa pori, akakuwa anakula majani kama ngombe, na kulowanishwa na umande wa mbinguni mpaka alipotambua kwamba Mungu Mukubwa ndiye anayetawala juu ya falme za wanadamu, naye anamupa ufalme ule mutu yeyote anayemutaka. Lakini wewe Belsasari mwana wake, ingawa unayajua haya yote, haukujinyenyekeza! Pahali pake umejitukuza mwenyewe mbele ya Bwana wa mbinguni: umeleta vyombo vya nyumba ya Mungu ukavitumia kwa kunywea divai, wewe, wakubwa wako, wanawake wako na wahabara wako, na kuisifu miungu iliyotengenezwa na feza, zahabu, shaba, chuma, miti na mawe; miungu ambayo haioni, haisikii wala haijui jambo lolote. Lakini Mungu, ambaye uzima wako uko katika mukono wake, na njia zako ziko wazi mbele yake, haukumuheshimu! Basi, Mungu ametuma mukono uandike maandiko haya. Maandiko yenyewe ni: MENE, MENE, TEKELI, PERESI. Na hii ndiyo maana yake. MENE: Mungu amehesabu siku za ufalme wako na kuukomesha. TEKELI: wewe umepimwa kwenye mizani, nawe ukaonekana hauna uzito wowote. PERESI: ufalme wako umegawanywa kati ya Wamedi na Wapersi. Pale pale, mufalme Belsasari akaamuru kwamba Danieli avalishwe nguo nzuri nyekundu na mukufu wa zahabu katika shingo. Ikatangazwa kwamba Danieli atakamata sasa nafasi ya tatu katika ufalme. Usiku uleule, mufalme Belsasari wa Wakaldea, aliuawa. Naye mufalme Dario, wa inchi ya Wamedi, akatwaa utawala akiwa na umri wa miaka makumi sita na miwili. Mufalme Dario aliamua kuweka wakubwa mia moja na makumi mbili kwa kusimamia mambo ya ufalme. Aliweka vilevile wakubwa watatu, Danieli akiwa mumoja kati yao, wawasimamie wale wakubwa wengine katika uongozi kusudi mufalme asipatwe na hasara. Danieli akaonekana kuwa bora kuliko wale wasimamizi wengine na wakubwa wote kwa maana alikuwa na roho njema. Hivyo mufalme akakusudia kumupa uongozi wa ufalme wote. Wale wakubwa pamoja na maliwali wakatafuta kisingizio cha kumushitaki Danieli juu ya mambo ya ufalme, lakini hawakuweza kupata sababu ya kumushitaki, wala kosa lolote, maana Danieli alikuwa mwaminifu. Hakupatikana na kosa, wala ubaya wowote. Halafu wakapatana hivi: Hatutapata kisingizio chochote cha kumushitaki Danieli isipokuwa kama kisingizio hicho kitakuwa kinaelekea Sheria ya Mungu wake. Basi, hao wakubwa na maliwali wote pamoja, wakamwendea mufalme na kumwambia: Uishi milele ee mufalme Dario! Sisi wakubwa uliotuweka, wasimamizi, maliwali, washauri na wakubwa wa majimbo, wote tumepatana kwamba inafaa, ee mufalme, utoe amri na kuhakikisha kwamba inafuatwa kikamilifu. Amuru kwamba kwa muda wa siku makumi tatu kusikuwe mutu yeyote atakayeruhusiwa kuomba kitu chochote kwa mungu yeyote au kwa mutu yeyote, isipokuwa kutoka kwako wewe, ewe mufalme. Mutu yeyote atakayevunja sheria hii atupwe katika pango la simba. Hivyo, ee mufalme Dario, utoe amri hiyo na kuitia sahihi yako kusudi isibadilishwe. Nayo itakuwa sheria ya Wamedi na Wapersi, sheria ambayo haitavunjika. Hivyo, mufalme Dario akatia sahihi kwenye sheria hiyo. Danieli alipojua kwamba ile sheria imetiwa sahihi, alirudi kwa nyumba yake kwenye gorofi katika chumba chake kilichokuwa na madirisha yaliyofunguka kuelekea Yerusalema. Humo, Danieli, kama ilivyokuwa kawaida yake, alipiga magoti mara tatu kila siku kwa kuomba na kumushukuru Mungu wake. Watu wale waliofanya mupango mubaya juu ya Danieli waliingia ndani, wakamukuta Danieli akiomba na kumusihi Mungu wake. Basi, walikwenda kwa mufalme na kumushitaki Danieli kwa kutumia ile sheria, wakisema: Mufalme Dario, haukutia sahihi kwenye sheria kwamba kwa muda wa siku makumi tatu hakuna mutu yeyote atakayeruhusiwa kuomba kitu chochote, kwa mungu yeyote, au kwa mutu yeyote isipokuwa kutoka kwako wewe, ee mufalme, na kwamba yeyote atakayevunja sheria hii atatumbukizwa katika pango la simba? Mufalme akaitikia: Hivi ndivyo inavyokuwa kulingana na sheria ya Wamedi na Wapersi ambayo haiwezi kuvunjika. Wakamwambia mufalme: Yule Danieli anayekuwa mumoja wa wafungwa kutoka inchi ya Yuda hakuheshimu wewe mufalme wala amri uliyotia sahihi. Anafanya maombi yake mara tatu kila siku. Mufalme aliposikia maneno hayo, alisikitika sana. Akafanya nguvu yake yote kwa kutafuta njia ya kumwokoa Danieli. Aliendelea kujaribu mpaka jua likatua. Wale watu kwa pamoja wakamwendea mufalme Dario na kumwambia: Ee mufalme, ujue kwamba hakuna sheria wala amri yoyote ya Wamedi na Wapersi inayoweza kubadilishwa kisha kuwekwa na mufalme. Halafu mufalme Dario akatoa amri, naye Danieli akaletwa na kutupwa katika pango la simba. Mufalme akamwambia Danieli: Mungu wako ambaye unamutumikia siku zote akuokoe. Jiwe likaletwa na kuwekwa kwenye mulango wa lile pango. Mufalme akapiga muhuri wake mwenyewe na ule wa wakubwa wake, kusudi uamuzi uliotolewa juu ya Danieli usibadilishwe. Kisha mufalme akarudi katika nyumba yake ya kifalme ambamo alikesha akifunga kula chakula wala hakupenda kufarijiwa na kitu chochote na hata usiku ule hakupata usingizi. Ilipokuwa asubui mapema, mufalme Dario aliamuka, akaenda kwa haraka kwenye pango la simba. Alipofika karibu akamwita Danieli kwa sauti ya huzuni: Danieli, mutumishi wa Mungu Mwenye Uzima, Mungu wako unayemutumikia siku zote ameweza kukuokoa na simba hawa? Danieli akamujibu mufalme: Uishi milele, ee mufalme! Mungu wangu alileta malaika wake kwa kufunga vinywa vya simba hawa, nao hawakunizuru. Alifanya hivyo kwa sababu alijua mimi sina kosa lolote mbele yake na wala sijafanya jambo lolote baya mbele yako. Kwa hiyo mufalme akafurahi sana; akaamuru kwamba wamwondoe Danieli toka ndani ya pango. Basi wakamwondoa, naye hakuonekana na alama hata kidogo ya kidonda, kwa sababu alimutegemea Mungu wake. Mufalme akaamuru wale watu waliomuchongea Danieli wakamatwe, nao wakatupwa ndani ya lile pango la simba pamoja na wake wao na watoto wao. Nao, hata mbele hawajagusa chini, simba waliwashambulia na kuivunjavunja mifupa yao. Halafu mufalme Dario akawaandikia watu wa makabila yote, mataifa yote, na luga zote katika dunia: Ninawatakia amani kwa wingi. Ninatoa amri katika ufalme wangu kwamba watu wote wanapaswa kumwogopa na kumuheshimu Mungu wa Danieli. Yeye ni Mungu Mwenye Uzima, anayeishi milele; ufalme wake hauwezi kuangamizwa hata kidogo, utawala wake hauna mwisho. Yeye anakomboa na kuokoa, anafanya miujiza na maajabu mbinguni na katika dunia, maana amemwokoa Danieli toka nguvu za simba. Basi, Danieli akastawi wakati wa utawala wa mufalme Dario na wa mufalme Kiro wa inchi ya Persia. Katika mwaka wa kwanza wa utawala wa mufalme Belsasari wa Babeli, Danieli aliota ndoto na kuona maono akiwa amelala katika kitanda chake. Akaandika ndoto yake hii: Mimi Danieli niliona maono usiku. Ilikuwa hivi: Upepo ulivuma juu ya bahari kubwa toka pande zote ine za mbinguni. Nyama wakubwa wane wakainuka kutoka ndani ya bahari, kila mumoja akiwa tofauti na mwenzake. Nyama wa kwanza alikuwa kama simba, na alikuwa na mabawa kama ya tai. Nikiwa ninamwangalia, mabawa yake yaliongolewa, naye akainuliwa na kusimama kwa miguu miwili kama mutu. Kisha, akapewa akili ya kimutu. Nyama wa pili alikuwa kama dubu ambaye upande wake mumoja ulikuwa umeinuka. Na katika kinywa chake alikuwa na mifupa mitatu ya mbavu aliyoishika kwa meno yake. Sauti ikamwambia: Simama, ukule nyama nyingi kadiri unavyoweza. Nyuma ya mambo hayo, nikaona nyama mwingine. Huyu alikuwa kama chui mwenye mabawa mane ya ndege juu ya mugongo wake. Alikuwa na vichwa vine naye alipewa uwezo wa kutawala. Kisha, katika maono hayo yangu ya usiku, nikaona nyama wa ine wa ajabu na wa kutisha, mwenye nguvu sana. Huyu alikuwa na meno makubwa ya chuma ambayo aliyatumia kwa kula na kuvunjavunja, na mabaki aliyakanyagakanyaga. Alikuwa tofauti na wale nyama wengine watatu, maana alikuwa na pembe kumi. Nilipokuwa ninaziangalia hizo pembe, niliona pembe ingine ndogo ikiota katikati ya zile kumi, nayo ikaongoa pembe tatu kati ya hizo za kwanza. Pembe ile ilikuwa na macho ya kimutu na kinywa kilichosema maneno ya kujivuna. Nilipokuwa nikiendelea kuangalia, nikaona viti vya kifalme viliwekwa hapo, kisha Muzee mumoja wa zamani sana akakuja, akaikaa. Alikuwa amevaa nguo nyeupe kama teluji; nywele zake zilikuwa kama sufu safi. Kiti chake cha kifalme kilikuwa ndimi za moto, na magurudumu ya kiti kile yalikuwa moto unaowaka. Kutoka kiti hicho kijito cha moto kilibubujika, kikatiririka. Maelfu ya watu walimutumikia, na mamilioni walisimama mbele yake. Halafu waamuzi wakajitayarisha kwa kuhukumu, na vitabu vikafunguliwa. Kutokana na maneno ya kujivuna yaliyokuwa yanasemwa na ile pembe, nikaendelea kuangalia. Nikaona yule nyama wa ine akiuawa, mwili wake ukaharibiwa na kutolewa uchomwe kwa moto. Wale nyama wengine walinyanganywa mamlaka yao, lakini wao wenyewe wakaachwa waendelee kuishi kwa muda fulani. Wakati wa maono haya usiku, niliona kiumbe kinachofanana na mwanadamu. Akakuja katika mawingu na kumwendea yule Muzee wa zamani sana. Akakaribishwa mbele yake. Akapewa mamlaka, utukufu na ufalme, kusudi watu wa makabila yote, mataifa yote na luga zote wamutumikie. Utawala wake ni wa milele na ufalme wake hautaangamizwa hata kidogo. Maono niliyoyaona mimi Danieli yaliniogopesha, nami nikafazaika. Nikajongea karibu na mutu mumoja kati ya wale waliosimama pale na kumwuliza maana kamili ya mambo hayo yote. Naye akanielezea maana yake akisema: Nyama hao wane wakubwa ni wafalme wane watakaotokea katika dunia. Lakini watakatifu wa Mungu Mukubwa watapewa ufalme, nao wataupokea ufalme huo milele na milele. Kisha nikataka nielezwe juu ya yule nyama wa ine, ambaye alikuwa tofauti kabisa na wale wengine, wa kutisha sana, mwenye meno ya chuma na makucha ya shaba, aliyekula na kuvunjavunja, na kukanyagakanyaga yaliyobaki. Vilevile nilitaka nielezwe juu ya zile pembe kumi alizokuwa nazo juu ya kichwa chake, na ile pembe moja iliyoota na pembe zingine tatu zilizoanguka mbele yake, ndiyo ile pembe iliyokuwa na macho na kinywa ambacho kilisema maneno ya kujivuna, na ambayo ilionekana kuwa kubwa kuliko pembe zingine. Nilipokuwa nikiangalia, pembe hio ilipigana vita na watakatifu, nayo ikawashinda. Lakini yule Muzee wa zamani sana akainuka, akawapa haki watakatifu wa Mungu na wakati ulipotimia, hao watakatifu wakapewa ufalme. Nilielezwa hivi: Yule nyama wa ine ni ufalme wa ine utakaokuwa katika dunia. Ufalme huo utakuwa tofauti na falme zingine, nao utaiangamiza dunia nzima. Utaiangusha chini na kuipasua vipandevipande. Zile pembe kumi ni wafalme kumi watakaotokana na ufalme huo. Halafu watafuatwa na mufalme mwingine ambaye atakuwa tofauti na wale waliomutangulia, na atawaangusha wafalme watatu. Huyo atasema maneno ya kujivuna mbele ya Mungu Mukubwa na kuwatesa watakatifu wake. Atajaribu kubadilisha sikukuu na sheria zao, na watakatifu watatiwa katika mikono yake kwa muda wa miaka mitatu na nusu. Lakini waamuzi watajitayarisha kwa kuamua watamunyanganya utawala wake, nao utafutwa na kuangamizwa kabisa. Ufalme, utawala na ukubwa wa falme zote katika dunia watapewa kwa watu wa watakatifu wa Mungu Mukubwa. Ufalme wao utakuwa wa kudumu milele, na tawala zote zitawatumikia na kuwatii. Huu ndio mwisho wa jambo hilo. Mawazo yangu yaliniogopesha sana mimi Danieli, hata rangi yangu ikabadilika. Lakini nilichunga jambo hilo ndani ya moyo wangu. Katika mwaka wa tatu wa utawala wa mufalme Belsasari, mimi Danieli nikapata maono mengine zaidi ya maono yale ya kwanza. Katika maono haya, nilijikuta niko Susani, muji mukubwa wa jimbo la Elamu. Nilikuwa nimesimama kando ya muto Ulayi. Nilipoinua macho yangu, niliona kondoo dume amesimama kando ya muto huo. Kondoo huyo alikuwa na pembe mbili ndefu, lakini moja ilikuwa ndefu zaidi, nayo ilitokea nyuma ya ile ingine. Nilimwona huyo kondoo dume akishambulia kuelekea upande wa magaribi, kaskazini na kusini. Hakuna nyama yeyote aliyesubutu kusimama mbele yake, wala kuziepuka nguvu zake. Alifanya sawa anavyopenda na kujitukuza mwenyewe. Nilipokuwa ninawaza juu ya jambo hili, niliona beberu mumoja kutoka upande wa magaribi akikuja mbio bila kugusa chini. Kati ya macho yake alikuwa na pembe moja kubwa sana. Alimwendea yule kondoo dume mwenye pembe mbili niliyemwona akiwa amesimama kando ya muto, akamushambulia kwa nguvu zake zote. Nilimwona akimusogelea yule kondoo dume. Alikuwa amemukasirikia sana yule kondoo dume, hivyo akamushambulia kwa nguvu na kuzivunja zile pembe zake mbili. Yule kondoo dume hakuweza kuvumilia. Aliangushwa chini na kukanyagwakanyagwa, wala hakuna yeyote kwa kumwokoa toka katika nguvu zake. Kwa hiyo yule beberu alijitukuza sana. Lakini alipofikia kilele cha nguvu zake, ile pembe yake kubwa ikavunjika. Pahali pake kukaota pembe ine zilizoonekana waziwazi, zikiwa zimeelekea pande ine za dunia. Na tokea ndani ya moja ya pembe hizo ine, kuliota pembe ingine dogo, ikakomaa sana kuelekea upande wa kusini-mashariki, na kuelekea inchi ile nzuri sana. Pembe dogo ile ilikomaa sana kufikia viumbe vya mbinguni; ikaangusha chini sehemu ya nyota na kuzikanyagakanyaga. Pembe dogo ile ikajitukuza mbele ya mukubwa wa viumbe vya mbinguni. Ikakomesha sadaka za kuteketezwa kwa moto ambazo mukubwa wa viumbe vya mbinguni alivyotambikiwa kila siku, na kuchafua hekalu lake. Viumbe vya mbinguni vikatiwa chini ya mamlaka yake pamoja na sadaka za kuteketezwa kwa moto za kila siku, kwa ajili ya upotovu. Nao ukweli ukatupwa chini. Pembe dogo ile ikaiangusha chini ibada ya kweli. Ilifanikiwa katika kila jambo iliyofanya. Kisha, nikamusikia mutakatifu mumoja akizungumuza na mwenzake. Huyo mwenzake alimwuliza: Matukio ya mambo yaliyotangazwa katika maono haya yataendelea kwa muda gani? Kwa muda gani sadaka za kuteketezwa za kila siku zitaendelea kuzarauliwa? Kwa muda gani upotovu wa kuangamiza kila kitu utaendelea, na Pahali Patakatifu pamoja na viumbe vya mbingu vitaendelea kukanyagwa? Yule mutakatifu wa kwanza akamujibu: Kwa muda wa nyakati za magaribi na asubui elfu mbili mia tatu. Kisha hekalu la Mungu litapata tena hali yake kamili. Mimi Danieli nilipoyaona maono hayo, na nilipokuwa nikijaribu kujua maana yake, kwa rafla, nikaona kiumbe kimoja chenye kufanana mwanadamu kikisimama mbele yangu. Nikasikia sauti ya mwanadamu kutoka katika muto Ulayi ikiita: Gabrieli, umwelezee mutu huyu maana ya maono aliyoona. Gabrieli akakuja karibu na pahali niliposimama. Mimi nikaogopa sana, hata nikaanguka uso mpaka chini. Lakini akaniambia: Wewe mutu, uelewe kwamba maono uliyoyaona yanaelekea wakati wa mwisho. Alipokuwa anazungumuza nami, mimi nikashikwa na usingizi muzito nikiwa nimelala uso mpaka chini. Lakini yeye akanishika na kunisimamisha. Kisha akaniambia: Sikiliza, ninakufahamisha jinsi matokeo ya kasirani ya Mungu yatakavyokuwa. Maono hayo yanaelekea wakati wa mwisho. Yule kondoo dume uliyemwona mwenye pembe mbili, ni wafalme wa Media na Persia. Yule beberu ni mufalme wa Ugriki. Ile pembe kubwa katikati ya macho yake ni mufalme wa kwanza. Ile pembe iliyovunjika na pahali pake kukaota pembe ine, ina maana kwamba ufalme huo mumoja utagawanyika kuwa falme ine, lakini falme hizo hazitakuwa na nguvu kama ule ufalme wa kwanza. Wakati falme hizo zitakapofikia kwa mwisho wao na uovu wao kufikia kilele chake, kutatokea mufalme mumoja mutesaji na mwerevu. Atakuwa mwenye mamlaka makubwa, atasababisha uharibifu mubaya sana, na atafanikiwa katika kila atakalotenda. Atawaangamiza watu wenye uwezo na watakatifu wa Mungu. Kwa werevu wake, atafanikiwa katika mipango yake ya udanganyifu, naye atajitukuza. Atawaangamiza watu wengi sana, na atataka kupigana na Mukubwa wa wakubwa, lakini ataangamizwa pasipo kutumia nguvu za kimutu. Maono ya hizo nyakati za magaribi na za asubui ambayo yameelezwa ni ya kweli. Lakini uyafiche, sababu ni siri, maana yatatokea kisha siku nyingi. Mimi Danieli, nikazimia na kuugua kwa muda. Nilipopona, nikaendelea na shuguli za mufalme. Lakini yale maono yalishangaza, nami sikuweza kuyaelewa. Katika mwaka Dario mufalme wa Wamedi mwana wa Ahasuero, alipoanza kutawala juu ya ufalme wa Wakaldea, mimi Danieli nilikuwa nikisoma kwa uangalifu vitabu vitakatifu, na humo nikaelewa maana ya jambo lile Yawe alilomufahamisha nabii Yeremia juu ya ile miaka makumi saba, muda ambao utahusika na kuharibiwa kwa Yerusalema. Nilimwomba Yawe, kwa moyo, nikimutolea maombi pamoja na kufunga kula chakula, nikavaa gunia na kuikaa kwenye majivu. Nilimwomba Yawe, Mungu wangu, na kuitikia zambi, nikisema: Ee Bwana, wewe ni Mungu mukubwa na wa kuogopesha. Wewe unashika agano lako na kutenda mema kwa wanaokupenda na kuzitii amri zako. Tumetenda zambi, tumekosa, tumetenda maovu na kukuasi. Tumevunja amri zako na maagizo yako. Hatukuwasikiliza watumishi wako manabii, ambao kwa jina lako walisema na wafalme wetu, wakubwa wetu, babu zetu na taifa letu lote. Kwako, ee Bwana, kuna haki, lakini sisi tumepata haya siku zote. Jambo hili ni kweli kwetu sisi wote tunaoishi Yudea, wakaaji wa muji Yerusalema na Waisraeli wote ambao umewatawanya katika inchi za mbali na za karibu kwa sababu ya kukosa uaminifu kwako. Ee Bwana, sisi tumefezeheka, wafalme wetu, wakubwa wetu na babu zetu, kwa sababu tumekutendea zambi. Wewe, Bwana Mungu wetu, una huruma na musamaha, ingawa sisi tumekuasi. Tulikataa kukusikiliza, ee Bwana wetu, Mungu wetu; hatukutenda kulingana na sheria zako ulizotupatia kwa njia ya watumishi wako manabii. Waisraeli wote wameiasi sheria yako, wamekuacha wakakataa kukutii. Kwa sababu tumekukosea, tumemwangiwa laana na viapo vilivyoandikwa katika Sheria ya Musa, mutumishi wako. Umetimiza yale uliyosema utatutendea sisi pamoja na watawala wetu kwa kuuazibu Yerusalema vikali zaidi ya muji mwingine wowote katika dunia. Umetuazibu kama ilivyoandikwa katika Sheria ya Musa, lakini mpaka sasa, ee Yawe, Mungu wetu, hatukuomba musamaha wako kwa kuziacha zambi zetu na kutambua uaminifu wako. Kwa hiyo, ee Yawe, Mungu wetu, ulikuwa tayari kutuazibu, na ukafanya hivyo, kwa sababu unafanya mambo yanayokuwa ya haki, nasi hatukukusikiliza. Na sasa ee Bwana, Mungu wetu, uliyewaondoa watu wako katika inchi ya Misri kwa nguvu yako kubwa na kulifanya jina lako litukuzwe mpaka sasa, tunasema kwamba tumetenda zambi; tumefanya maovu. Ee Bwana, kwa kadiri ya matendo yako ya haki usiukasirikie wala kuwa na hasira kwa ajili ya muji wako Yerusalema, mulima wako mutakatifu. Watu wote wa inchi za jirani wanauzarau Yerusalema na watu wako, kwa sababu ya zambi zetu na maovu babu zetu waliyotenda. Kwa hiyo, ee Mungu, usikilize malalamiko yangu na maombi yangu mimi mutumishi wako. Kwa ajili ya heshima yako, ulionee tena hekalu lako lililoharibika huruma. Tega sikio, ee Mungu wangu; angalia uone taabu tunazokuwa nazo na jinsi huo muji unaoitwa kwa jina lako unavyotaabika. Tunakutolea maombi yetu si kwa sababu tumetenda haki, lakini kwa sababu wewe una huruma nyingi. Ee Yawe, utusikie; utusamehe ee Yawe. Ee Yawe, kwa ajili ya heshima yako utusikie na utende, wala usikawie, ee Mungu wangu, kwa ajili ya muji huu na watu hawa wanaoitwa kwa jina lako! Basi, nilipokuwa nikiomba, nikiitikia zambi zangu na zambi za watu wangu wa inchi ya Israeli, pamoja na kumusihi Yawe kwa ajili ya mulima wake mutakatifu, yule mutu Gabrieli, ambaye nilikuwa nimemwona katika maono hapo mbele, alishuka kwa haraka mpaka pahali nilipokuwa. Ilikuwa wakati wa kutoa sadaka ya magaribi. Basi, akaniambia: Danieli, nimekuja kukupa hekima na uwezo wa kufahamu. Ulipoanza kuomba, Mungu alitoa jibu, nami nimekuja kukuelezea jibu hilo kwa sababu unapendwa sana. Kwa hiyo, usikilize kwa uangalifu jibu hilo na kuelewa maono hayo. Muda wa miaka saba mara makumi saba umewekwa kwa ajili ya watu wako na juu ya muji wako mutakatifu kwa kumaliza makosa, kukomesha zambi, kusamehe uovu, kuleta haki ya milele, kutia muhuri juu ya maono na unabii na kupakaa mafuta katika Pahali Patakatifu Sana. Basi, ujue na kufahamu jambo hili: tangu wakati amri itakapotolewa ya kujengwa upya Yerusalema mpaka kuja kwa yule aliyepakwa mafuta, yule anayekuwa mukubwa, ni muda wa majuma saba. Kwa muda wa majuma makumi saba na mawili, Yerusalema utajengwa upya, wenye barabara kubwa na kuta, lakini wakati huo utakuwa wa taabu. Kisha majuma hayo makumi saba na mawili, yule aliyepakwa mafuta atauawa na hatabaki na kitu. Muji na Pahali Patakatifu Sana vitaharibishwa na waaskari wa mutawala atakayekuja kushambulia. Mwisho wake utafika kama mafuriko, kukiwa vita na maangamizi kama yalivyopangwa na Mungu. Mutawala huyo atafanya mapatano imara na watu wengi kwa muda wa miaka saba. Kisha nusu ya muda huo atakomesha sadaka za kuteketezwa kwa moto na sadaka zingine. Pahali pa juu katika hekalu patasimamishwa chukizo linaloleta uharibifu, nalo litabaki pale mpaka yule aliyemusimamisha atakapoangamizwa kama ilivyopangwa na Mungu. Katika mwaka wa tatu wa utawala wa mufalme Kiro wa Persia, Danieli, aliyeitwa vilevile Beltesaza, alipewa ufunuo. Ufunuo huo ulikuwa wa kweli, lakini ulikuwa mugumu sana. Hata hivyo alielewa ufunuo huo maana alifahamu maono vilevile. Wakati huo, mimi Danieli, nilikuwa nikiomboleza kwa muda wa majuma matatu. Sikukula chakula kizuri, sikugusa nyama wala divai, na sikujipakaa mafuta kwa muda wa majuma hayo yote matatu. Siku ya makumi mbili na ine ya mwezi wa kwanza, nilikuwa nimesimama kando ya muto Tigre. Nikainua macho, nikamwona mutu anayevaa nguo za kitani naye alikuwa amejifunga mukaba wa zahabu safi kutoka Ufasi. Mwili wake ulingaa kama zabarajadi safi. Uso wake ulifanana na umeme, na macho yake yaliwaka kama ndimi za moto. Miguu na mikono yake ilingaa kama shaba iliyosafishwa sana. Sauti yake ilivuma kama sauti ya kundi kubwa la watu. Mimi Danieli peke yangu niliona maono hayo. Wale watu waliokuwa pamoja nami hawakuyaona, lakini walishikwa na hofu sana, wakakimbia, wakajificha. Hivyo, niliachwa peke yangu nikiangalia hayo maono ya kushangaza. Nguvu zikaniishia, na uso wangu ukabadilika rangi, nikabaki bila nguvu. Nilipoisikia sauti yake, nilianguka uso mpaka chini, nikashikwa na usingizi muzito. Hapo, mukono ukanigusa, ukanisimamisha, na kuimarisha miguu na mikono yangu. Akaniambia: Danieli, wewe unayependwa sana, simama sawa usikilize kwa uangalifu maneno nitakayosema, maana nimetumwa kwako. Alipokuwa akiniambia maneno haya, mimi nilisimama nikitetemeka. Kwa hiyo yeye akaniambia: Danieli, usiogope. Mungu alisikia maombi yako tangu siku ile ya kwanza ulipoamua kujinyenyekeza mbele yake kusudi upate ufahamu. Mimi nimekuja kwa ajili ya maombi yako hayo. Mukubwa wa ufalme wa Persia alinipinga kwa muda wa siku makumi mbili na moja. Lakini Mikaeli, mumoja kati ya wakubwa, akakuja kunisaidia, kwa hiyo nikamwacha kule pamoja na mukubwa wa ufalme wa Persia, nami nimekuja kukusaidia upate kuyafahamu mambo yatakayowapata watu wako wakati unaokuja, maana maono uliyoona yanaelekea wakati unaokuja. Alipokuwa ananiambia maneno hayo, niliangalia chini bila kuweza kusema. Kisha, kiumbe kimoja chenye umbo la mutu, kiliigusa midomo yangu, nami nilifungua midomo yangu na kumwambia huyo aliyesimama karibu nami: Ee bwana, maono haya yameniletea maumivu makali hata nimeishiwa nguvu. Mimi ni kama mutumwa mbele ya bwana wake. Ninaweza namna gani kusema nawe? Sina nguvu na pumzi imeniishia! Yule aliyeonekana kama mwanadamu akanigusa kwa mara ingine, akanitia nguvu. Akaniambia: Usiogope wewe unayependwa sana, uko salama. Ukuwe imara na hodari. Aliposema nami, nilipata nguvu, nikamwambia: Bwana, umekwisha kuniimarisha; sema kile ulichotaka kusema. Naye akaniambia: Unajua kwa nini nimekuja kwako? Sasa ninapaswa kurudi kwenda kupigana na malaika mulinzi wa Persia. Halafu, nitakapokuwa nimemushinda, malaika mulinzi wa mufalme wa Ugriki atatokea. Lakini nitakujulisha yale yaliyoandikwa katika kitabu cha ukweli. Sina mwingine wa kunisaidia kwa kuwashinda hawa isipokuwa Mikaeli, malaika mulinzi wenu. Lakini kwa upande wangu mimi, katika mwaka wa kwanza wa utawala wa mufalme Dario wa Wamedi, nilijitoa kwa kumuimarisha na kumutia nguvu. Sasa nitakuelezea ule ukweli wa mambo haya. Wafalme wengine watatu wataitawala inchi ya Persia. Hao watafuatwa na mufalme wa ine ambaye atakuwa tajiri kuliko wale waliomutangulia. Wakati atakapopata nguvu kwa ajili ya utajiri wake, ataanza kuushambulia ufalme wa Ugriki. Kisha kutatokea mufalme hodari atakayetawala eneo kubwa na kufanya atakavyopenda. Hata hivyo, wakati atakapokuwa na nguvu, ufalme wake utavunjika na kugawanyika katika sehemu ine kuelekea pande ine za mbingu. Wazao wake hawatatawala, wala ufalme hautakuwa katika mikono ya urizi aliotawala, kwa sababu ufalme wake utakamatwa na wengine. Mufalme wa kusini atakuwa mwenye nguvu. Lakini mumoja wa majemadari wake atakuwa na nguvu kuliko yeye na utawala wake utakuwa mukubwa zaidi. Kisha miaka michache, wataungana pamoja; binti wa mufalme wa kusini ataolewa katika jamaa ya mufalme wa kaskazini na kutimiza mapatano hayo, lakini hataendelea kuwa na nguvu, hata mufalme na wazao wake hawatavumilia; na huyo binti, mwana wake na wajakazi aliokwenda nao, wote watauawa. Kisha mutoto mumoja wa ukoo wa huyo binti atakuwa mufalme. Huyo atayashambulia makundi ya waaskari wa mufalme wa kaskazini na kuingia katika miji yao yenye kuzungukwa na kuta na kushinda. Atabeba sanamu za miungu yao na vyombo vya bei kali vya feza na zahabu mpaka katika inchi ya Misri. Kwa muda wa miaka michache, mufalme wa kusini hatamushambulia mufalme wa kaskazini. Lakini nyuma, mufalme huyu wa kaskazini ataushambulia ufalme wa kusini, kisha atarudi katika inchi yake. Wana wa mufalme wa kaskazini watakusanya kundi kubwa la waaskari na kujitayarisha kwa vita. Kundi hilo litasonga mbele kama mafuriko ya maji litapita na kupigana vita mpaka ndani ya muji wenye kuta wa waadui. Halafu, mufalme wa kusini, kwa hasira yake, atapigana vita na mufalme wa kaskazini ambaye naye atamushambulia kwa kundi kubwa la waaskari, lakini litashindwa. Kisha kulishinda vibaya kundi la waasakri wa kaskazini na kuua maelfu, ataanza kujisifu, lakini hataendelea kuwa mushindi. Maana kwa mwisho mufalme wa kaskazini atatayarisha kundi kubwa la waaskari kuliko lile la mbele. Kisha miaka michache atarudi na kundi kubwa la waaskari lenye vifaa vingi vya vita. Wakati huo watu wengi watamwasi mufalme wa kusini. Watu wamoja waovu wa taifa lako wewe Danieli, wataasi kwa kutimiza maono haya, lakini watashindwa. Halafu mufalme wa kaskazini atalundika udongo kando ya muji wenye kuta imara na kuuteka. Waaskari wa kusini hawataweza kuupiganisha, hata wale wafundi wa vita, maana hawatakuwa na nguvu. Mushambulizi atawatendea sawa anavyopenda; hakuna atakeyesubutu kupingana naye. Atasimama katika inchi tukufu, na inchi hiyo yote itakuwa chini ya mamlaka yake. Huyo mushambulizi atakusudia kuja na kundi lake lote la waaskari, naye atafanya mapatano na kuyatimiza. Atamuoesha binti yake mumoja kusudi apate kuuangamiza ufalme wa adui yake; lakini mupango wake hautawezekana, wala kumufaidia kwa jambo lolote. Nyuma ya hayo, atageukia na kushambulia inchi nyingi za kandokando ya bahari na kuzishinda. Lakini jemadari mugeni atamushinda na kuyakomesha majivuno yake mwenyewe; kweli atamurudishia mufalme wa kaskazini majivuno yake mwenyewe. Halafu atageuka kurudi katika kuta za inchi yake mwenyewe, lakini atajikwaa na kuanguka katika vita na huo ndio utakaokuwa mwisho wake. Huyu atafuatwa na mufalme mwingine ambaye atatuma mulipishaji wa kodi kupita katika nafasi ya utukufu ya ufalme wake. Mufalme huyo atauawa kisha siku chache, lakini si kwa hasira wala katika vita. Mufalme atakayefuata atakuwa wa kuzarauliwa ambaye asiyeweza kupewa heshima ya kifalme, naye atakuja wakati watu wasiouzania na kunyanganya ufalme kwa werevu. Makundi ya waaskari pamoja na kuhani wa hekalu wataangamizwa na kuwaua. Kwa kufanya mapatano, atayadanganya mataifa mengine, na ataendelea kupata nguvu ingawa atatawala taifa dogo. Na kwa wakati wasiouwazia ataingia katika sehemu za jimbo zenye utajiri mwingi na kufanya mambo ambayo hayakufanyika hata na mumoja wa babu zake waliomutangulia. Kisha, atawagawanyia wafuasi wake mali na vitu alivyonyanganya katika vita. Atafanya mipango ya kuishambulia miji yenye kuta, lakini kwa muda tu. Kwa uhodari mwingi, ataunda kundi kubwa la waaskari kusudi apate kuushambulia ufalme wa kusini, naye mufalme wa kusini atajibu mashambulizi hayo kwa kundi kubwa zaidi la waaskari na lenye nguvu sana. Lakini, mufalme wa kusini hatashinda kwa maana watafanya shauri baya juu yake. Wale wanaokula pamoja naye, ndio watakaomwangamiza. Watamwangamiza na waaskari wake watasambazwa na wengi watauawa. Halafu wafalme hao wawili wataikaa kwa meza pamoja, lakini kila mumoja anamuwazia mwenzake uovu, na kudanganyana. Lakini hawatafanikiwa, maana wakati uliopangwa utakuwa bado haujatimia. Mufalme wa kaskazini atarudi katika inchi yake akiwa na mali nyingi, lakini nia yake ndani ya moyo ni kulivunja agano takatifu. Atafanya vile anavyopenda, kisha atarudi katika inchi yake. Katika wakati uliopangwa ataishambulia inchi ya kusini kwa mara ingine, lakini mara hii, mambo yatakuwa tofauti. Mashua kutoka Kitimu zitamushambulia, naye atashikwa na hofu. Kisha atarudi nyuma akiwa amejaa hasira na kuvunja agano takatifu. Halafu atafuata shauri la wale walioasi agano takatifu. Waaskari wake watalichafua hekalu na kuta zake, watakomesha sadaka za kuteketezwa kwa moto za kila siku na kusimamisha kule katika hekalu chukizo linaloleta uharibifu. Atawashawishi kwa werevu wale walioasi agano, lakini watu wanaokuwa waaminifu kwa Mungu wao watasimama imara na kutenda. Wenye hekima kati ya watu watawafundisha wengi. Hata hivyo, kwa siku chache watauawa kwa upanga au kwa moto, watakamatwa mateka au kunyanganywa mali zao. Wakati wanapouawa, watapata musaada kidogo, na wengi wanaojiunga nao, watafanya hivyo kwa unafiki. Wamoja kati ya wenye hekima watauawa, kusudi wapate kuondolewa uchafu, kutakaswa na kusafishwa, mpaka wakati wa mwisho, ambao sasa bado haujatimia. Mufalme atafanya kama anavyopenda. Atajitukuza na kujivuna kwamba yeye ni mukubwa kuliko miungu yote, na kumutukana Mungu wa miungu. Ataendelea kufanikiwa mpaka kasirani ifikie ukomo wake, maana yaliyopangwa sherti yatimie. Mufalme huyo hataijali miungu ya babu zake wala yule anayependwa na wanawake. Ataizarau miungu mingine yote, maana atajiweka kuwa mukubwa kuliko kila mumoja wao. Pahali pa miungu hiyo atamuheshimu mungu mulinzi wa kuta za muji, ambaye babu zake hawakumwabudu hata kidogo. Atamutolea zahabu, feza na mawe ya bei kali, na zawadi za bei kubwa. Atazishugulikia kuta za muji wake kwa musaada wa mungu wa kigeni. Wale wanaomutambua kuwa mufalme, atawaongezea heshima kubwa, atawapa vyeo vikubwa na kuwagawanyia inchi kama zawadi. Wakati wa mwisho mufalme wa kusini atamushambulia mufalme huyo wa kaskazini. Lakini mufalme wa kaskazini atajibu mashambulio hayo kwa nguvu kama zoruba, akitumia magari ya vita, waaskari wapanda-farasi na mashua nyingi. Atashambulia inchi nyingi na kupita katika inchi hizo kama mafuriko ya maji. Atashambulia hata inchi ile tukufu na kuua maelfu ya watu. Lakini inchi za Edomu, Moabu na sehemu kubwa ya Amoni, zitaokoka kutoka katika mikono yake. Wakati atakaposhambulia inchi hizo, hata inchi ya Misri haitaponyoka. Atatwaa akiba za zahabu, feza na mawe yote ya bei kali ya inchi ya Misri. Watu wa Libya na watu wa Etiopia watamufuata. Lakini habari kutoka mashariki na kaskazini zitamutisha. Naye atatoka kwa hasira kubwa kusudi aharibu na kuangamiza watu wengi. Zaidi ya hayo, atapiga mahema yake makubwa kati ya bahari na mulima mutukufu na mutakatifu. Lakini atakuwa amefikia ukomo wake, na hakutakuwa mutu yeyote wa kumusaidia. Wakati huo, Mikaeli, malaika mukubwa, anayekuwa mulinzi wa watu wako, atatokea. Halafu kutakuwa wakati wa taabu sana kuliko nyakati zingine zote tangu mataifa yalipoanza kuwa katika dunia. Lakini, wakati huo, kila mumoja wa watu wako ambaye jina lake limeandikwa katika kitabu cha uzima, ataokolewa. Wengi wa wale ambao wamekwisha kufa, watafufuka; wengine watapata uzima wa milele, na wengine watapata haya na kuzarauliwa milele. Wale wenye hekima watangaa kama vile anga linavyongaa, na wale waliowaongoza wengine kutenda mema, watangaa kama nyota milele. Lakini sasa, Danieli, weka kwa siri mambo hayo; funga kitabu na kutia muhuri juu yake mpaka wakati wa mwisho utakapofika. Wengi watakimbilia huko na huko, na maarifa yataongezeka. Kisha, mimi Danieli nikaangalia, nikaona watu wawili wakisimama kwenye ukingo wa muto; mumoja upande huu na mwingine upande wa pili. Nikamwuliza yule aliyesimama upande wa juu wa muto, aliyevaa nguo za kitani: Mambo haya ya kutisha yatadumu mpaka wakati gani? Yule mutu aliyesimama upande wa juu wa muto, aliyevaa nguo za kitani, akainua mikono yake yote miwili kuelekea mbinguni. Kisha nikamusikia akiapa kwa jina la yule anayeishi milele: Itakuwa muda wa nyakati tatu na nusu. Wakati mateso ya watu watakatifu yatakapokomeshwa, mambo haya yote yatakuwa yametimia. Nilisikia lakini sikuelewa. Halafu, nikamwuliza: Bwana wangu, mwisho wa mambo haya yote utakuwa namna gani? Akanijibu: Danieli, ujiendee, maana maneno haya ni siri na yamefungwa kwa kutiwa muhuri juu yake mpaka wakati wa mwisho. Watu wengi wataondolewa uchafu, watatakaswa na kusafishwa. Lakini watu waovu wataendelea kutenda uovu. Hakuna hata mumoja wa hao waovu atakayeelewa; wenye hekima ndio watakaoelewa. Tangu wakati wa kukomeshwa kwa sadaka za kuteketezwa kwa moto za kila siku, ni kusema kutoka wakati ule chukizo linaloleta uharibifu litakaposimamishwa, itakuwa muda wa siku elfu moja mia mbili na makumi kenda. Heri yao watakaovumilia mpaka siku zile elfu moja mia tatu na makumi tatu na tano zitakapotimia. Lakini wewe, ee Danieli, ujiendee, upumzike katika kaburi, na wakati huo utakapotimia, utafufuka na kupata zawadi yako. Hili ni neno ya Yawe lililomufikia Hosea mwana wa Beri katika siku za utawala wa Uzia, Yotamu, Ahazi na Hezekia, wafalme wa Yuda, na Yeroboamu mwana wa Yoasi, mufalme wa Israeli. Yawe alipoanza kusema na Waisraeli kwa njia ya Hosea, alimwambia hivi: Kwenda kuoa mwanamuke muzinzi, uzae naye watoto wa uzinzi, maana watu wa inchi hii wanafanya uzinzi mwingi kwa kuniacha mimi. Basi, Hosea akaenda, akamwoa Gomeri, binti wa Dibulaimu. Gomeri akapata mimba, akamuzalia Hosea mutoto mwanaume. Yawe akamwambia Hosea: Umupange mutoto huyo jina la “Yezereheli”, maana kisha siku chache tu, nitaiazibu jamaa ya Yehu kwa mauaji aliyofanya katika bonde la Yezereheli. Hivi nitavunja ufalme katika taifa la Israeli. Siku hiyo, nitazivunja nguvu za makundi ya waaskari wa Israeli kule katika bonde la Yezereheli. Gomeri alipata mimba tena, akazaa mutoto mwanamuke. Yawe akamwambia Hosea: Umupange mutoto huyo jina la “Asiyehurumiwa”, maana sitawahurumia tena Waisraeli wala sitawasamehe. Lakini nitawahurumia watu wa Yuda na kuwaokoa. Mimi Yawe, Mungu wao, nitawaokoa, lakini si kwa nguvu za waaskari, au pinde, au panga, au farasi au waaskari wapanda-farasi. Gomeri alipomwachisha yule binti wake Asiyehurumiwa kunyonya, alipata mimba tena, akazaa mutoto mwingine mwanaume. Yawe akamwambia Hosea: Umupange mutoto huyo jina la “Si wangu”, maana ninyi si watu wangu, wala mimi si Mungu wenu. Lakini hesabu ya Waisraeli itakuwa kubwa kama muchanga wa bahari ambao haupimiki wala hauhesabiki. Pale ambapo Mungu aliwaambia: Ninyi si watu wangu, sasa atawaambia: Ninyi ni watoto wa Mungu Mwenye Uzima. Watu wa Yuda na Waisraeli wataungana pamoja na kumuchagua mwongozi wao mumoja; nao watastawi katika inchi yao. Hiyo itakuwa siku kubwa ya Yezereheli. Basi, muwaite wakaka zenu, “Watu wangu”, na wadada zenu, “Waliohurumiwa”. Mumushitaki mama yenu, mumushitaki, maana sasa yeye si muke wangu wala mimi si mume wake. Mumushitaki aondoe vitambulisho vya uasherati juu ya uso wake, ajiepushe na mapambo ya uzinzi juu ya kifua chake. Kama sivyo, nitamuvua nguo abaki uchi, nitamufanya akuwe sawa vile alivyozaliwa. Nitamufanya akuwe utupu sawa jangwa, akauke sawa inchi kavu. Nitamwua kwa kiu. Na watoto wake sitawahurumia, maana ni watoto wa uzinzi. Mama yao amefanya uzinzi, aliyebeba mimba yao amefanya mambo ya haya. Alisema: Nitaambatana na wapenzi wangu, ambao wananipatia chakula na maji, nguo za sufu na kitani, pamoja na mafuta na divai. Basi, nitafunga njia yake kwa miiba, nitamuzungushia ukuta, asipate njia ya kutokea inje. Atawafuata wapenzi wake, lakini hatawapata; atawatafuta, lakini hatawaona. Kwa hiyo atasema: Nitarudi kwa mume wangu wa kwanza; maana zamani nilikuwa na raha kuliko sasa. Hakujua kwamba ni mimi niliyemupa ngano, divai na mafuta, niliyemujalia feza na zahabu kwa wingi, ambazo alimupelekea mungu Bali. Kwa hiyo wakati wa mavuno nitaitwaa ngano yangu, nitaiondoa divai yangu kwa wakati wake. Nitamunyanganya nguo zangu za sufu na kitani, ambazo zilitumika kuufunika uchi wake. Nitamuvua nguo abaki uchi mbele ya wapenzi wake, wala hakuna mutu atakayeweza kunizuia. Nitakomesha furaha zake zote, sikukuu zake za mwandamo wa mwezi na za Sabato, na sikukuu zote zilizoamriwa. Nitaiharibu mizabibu yake na tini zake, anayosema ni malipo kutoka kwa wapenzi wake. Nitaifanya ikuwe pori, nao nyama wa pori wataikula. Nitamulipiza kwa ajili ya siku alizoabudu sanamu za mungu Bali, kwa ajili ya muda alioutumia kuzifukizia ubani, akajipamba kwa pete zake na ushanga, na kuwaendea wapenzi wake, akanisahau mimi. –Ni ujumbe wa Yawe. Kwa hiyo, nitamushawishi, nitamupeleka katika jangwa na kusema naye kwa upole. Huko nitamurudishia mashamba yake ya mizabibu. Bonde la Akori litakuwa mulango wa tumaini. Ataniitikia vizuri kama vile alipokuwa kijana, kama wakati alipotoka katika inchi ya Misri. Siku hiyo, wewe utaniita “Mume wangu”, na sio tena “Bali wangu”. –Ni ujumbe wa Yawe.– Maana, nitalifanya jina la Bali lisitajike tena katika kinywa chako. Nitafanya agano na nyama wa pori, ndege pamoja na vyote vinavyotambaa, kusudi wasikuumize. Nitaondoa upinde, upanga na silaha za vita katika inchi, na kukufanya uishi kwa usalama. Nitakufanya muke wangu milele; ukuwe wangu kwa sheria na haki, kwa wema na huruma. Kweli, nitakuoa kwa uaminifu, nawe utanijua mimi Yawe. Siku hiyo, nitajibu kwa mahitaji ya mbingu ya kunyesha mvua, mbingu nazo zitajibu kwa mahitaji ya udongo. –Ni ujumbe wa Yawe.– Udongo utajibu mahitaji ya ngano, divai na mafuta, navyo vyote vitajibu kwa mahitaji ya Yezereheli. Nitamwotesha Yezereheli katika inchi; nitamuhurumia yule aliyeitwa “Asiyehurumiwa”, na wale walioitwa “Si wangu”, nitawaambia: “Ninyi ni watu wangu”. Nao watasema: Wewe ni Mungu wetu. Yawe akaniambia: Kwenda tena umupende mwanamuke anayependwa na mwanaume mwingine na ambaye ni muzinzi. Umupende kama vile mimi Yawe ninavyowapenda Waisraeli, ingawa wao wanaigeukia miungu mingine na kupenda mikate ya zabibu. Basi, nikamupata huyo mwanamuke kwa vikoroti kumi na vitano vya feza na saki nyingi za shayiri. Kisha nikamwambia: Unapaswa kuwa wangu kwa siku nyingi bila kufanya uzinzi au kuwa muke wa mutu mwingine; nami vilevile nitakuwa mwaminifu. Hivi ndivyo Waisraeli watakavyokuwa: watakaa kwa muda murefu bila mufalme au mukubwa; bila sadaka, wala nguzo za sanamu wala vyombo walivyotumia kwa kujua mapenzi ya Mungu. Nyuma, Waisraeli watarudi na kumutafuta Yawe, Mungu wao, na kumutafuta mufalme wao, wa uzao wa Daudi. Halafu watamutii Yawe, na kutazamia wema wake siku za mwisho. Musikilize maneno ya Yawe, enyi Waisraeli. Yawe anawashitaki wakaaji wa inchi hii. Hakuna tena uaminifu wala wema katika inchi; hakuna anayemujua Mungu katika inchi hii. Kuapa, uongo, mauaji, wizi na uzinzi vinatokea humo. Umwangaji wa damu unafuatana kwa mufululizo. Kwa hiyo, inchi yote inakauka, wakaaji wake wote wanaangamia pamoja na nyama na ndege; hata samaki wanaangamizwa. Lakini watu wasilaumiwe, wasishitakiwe; maana mimi ninakushitaki wewe kuhani. Wewe utajikwaa muchana, naye nabii atajikwaa pamoja nawe usiku. Nitamwangamiza mama yako Israeli. Watu wangu wameangamia kwa kutonijua, maana wewe kuhani umekataa mafundisho. Nimekukataa kuwa kuhani wangu. Kwa maana umeisahau sheria ya Mungu wako, nami vilevile nitawasahau watoto wako. Kadiri makuhani walivyoongezeka, ndivyo wote walivyozidi kuniasi. Basi, nitageuza utukufu wao kuwa haya. Wanajishibisha kwa sadaka za watu wangu wenye zambi. Wana hamu sana ya kuwaona wakitenda zambi. Lakini yatakayowapata watu yatawapata makuhani; nitawaazibu kwa sababu ya mwenendo wao, nitawalipiza matendo yao wenyewe. Watakula, lakini hawatashiba, watazini, lakini hawatapata watoto, kwa sababu wameniacha mimi Yawe, na kufuata miungu mingine. Uasherati, divai mupya na ya zamani vinaondoa maarifa. Watu wangu wanaomba shauri kutoka kwa muti; kijiti chao cha kuaguza ndicho kinachowapa shauri. Nia ya kufanya uzinzi imewapotosha; wamefanya uzinzi kwa kufuata miungu mingine, wakaniacha mimi Mungu wao. Wanatambikia kwenye vilele vya milima; wanatoa sadaka kwenye vilima, chini ya miti ya mwalo, migude na mikwaju, maana kivuli chao ni kizuri. Kwa hiyo wabinti wenu wanafanya uzinzi, na bibi-arusi wenu anafanya uasherati. Lakini sitawaazibu wabinti zenu wanapofanya uzinzi, wala bibi-arusi wenu wanapofanya uasherati, maana, wanaume wenyewe ndio wanaofuatana na wazinzi, na kutambikia pamoja nao katika ibada za uzinzi. Watu hawa wenye kukosa akili hakika wataangamia! Ikiwa kweli ninyi Waisraeli ni wazinzi lakini, watu wa Yuda basi wasianguke ndani ya makosa! Musiende pahali patakatifu kule Gilgali, wala musiende kule Nyumba ya Uovu. Wala musiape mukisema: Kama vile Yawe anavyoishi! Waisraeli ni wenye kichwa kigumu kama punda. Kwa nini basi Mungu ashugulike na kuwachunga, kama kondoo katika shamba kubwa la kuwakulishia? Watu wa Efuraimu wamejiunga na sanamu. Basi! Uwaache waendelee tu! Kama vile kundi la walevi, wanajizamisha wenyewe katika uzinzi; wanapendelea mambo ya haya kuliko heshima yao. Basi, zoruba itawapeperusha, nao watapata haya kwa ajili ya sadaka zao. Musikilize, enyi makuhani! Mutege sikio, enyi Waisraeli! Musikilize, enyi ukoo wa kifalme! Ninyi mulipaswa kulinda haki, pahali pake mumekuwa kama mutego kule Misipa, mumekuwa kama wavu wa kuwanasa kule Tabori. Mumechimba shimo refu la kuwanasa kule Sitimu. Lakini mimi nitawaazibu ninyi wote. Ninawajua watu wa Efuraimu, Waisraeli hawakufichwa kwangu. Ninyi watu wa Efuraimu mumefanya uzinzi, watu wote wa Israeli wamejichafua. Matendo yao yanawazuia wasimurudilie Mungu wao. Wamejaa uzinzi ndani ya mioyo yao; hawanijui mimi Yawe. Kiburi cha Waisraeli kinaonekana wazi; watu wa Efuraimu watajikwaa katika makosa yao, nao watu wa Yuda watajikwaa pamoja nao. Watakwenda na makundi yao ya kondoo na ngombe, kumutafuta Yawe; lakini hawataweza kumupata, kwa sababu amejitenga nao. Wamevunja uaminifu kwa Yawe, wamezaa watoto wa haramu. Mwezi mumoja utatosha kwa kuwaangamiza, pamoja na mashamba yao. Mupige baragumu kule Gibea, na ngunga kule Rama. Mupige kelele la kujulisha hatari kule Beti-Aweni. Enyi watu wa Benjamina, adui yenu yuko nyuma! Siku nitakapotoa azabu, Efuraimu itakuwa kama jangwa! Ninachotangaza kati ya makabila ya Israeli, ni jambo litakalotukia kwa hakika. Waongozi wa Yuda wamekuwa wenye kubadilisha mipaka ya inchi. Mimi nitawamwangia hasira yangu kama maji. Efuraimu ameteswa, haki zake zimetwaliwa; maana alikusudia kufuata mambo isiyokuwa na maana. Hivyo mimi Mungu niko kama nondo kwa Efuraimu, kama kidonda kibaya kwa watu wa Yuda. Watu wa Efuraimu walipogundua ugonjwa wao, watu wa Yuda walipogundua kidonda chao, watu wa Efuraimu walikwenda Asuria kuomba musaada kwa mufalme mukubwa; lakini yeye hakuweza kuwatunza, hakuweza kuponyesha kidonda chao. Maana mimi nitakuwa kama simba kwa Efuraimu, kama simba mukali kwa watu wa Yuda. Mimi mwenyewe nitawararua na kuondoka, nitawakamata na hakuna atakayewaokoa. Nitarudi mahali pangu na kujitenga nao mpaka watambue kosa lao na kunirudilia. Taabu zao zitawafundisha wanitafute. Halafu watasema: Tuende tumurudilie Yawe! Yeye mwenyewe ameturarua, lakini yeye mwenyewe atatuponyosha. Yeye mwenyewe ametuumiza, lakini yeye mwenyewe atatunza vidonda. Nyuma ya siku mbili atatupatia tena uzima. Nyuma ya siku tatu atatufufua kusudi tuweze kuishi pamoja naye. Basi tumutambue, tujikaze sana kumujua Yawe. Kuja kwake ni hakika kama mapambazuko, yeye atatufikia kama vile manyunyu, kama vile mvua za kwanza zinavyolowanisha udongo. Lakini Yawe anasema hivi: Nitakutendea nini, ee Efuraimu? Nikufanyie nini, ee Yuda? Upendo wenu kwangu ni kama ukungu wa asubui, kama umande unaotoweka upesi. Ndiyo maana ninawashambulia kwa njia ya manabii, nimewaangamiza kwa maneno yangu, hukumu yangu inajitokeza kama mapambazuko. Maana kitu ninachotaka kwenu ni wema na si sadaka, kumujua Mungu na si kutoa sadaka za kuteketezwa kwa moto. Lakini mulivunja agano langu kama mulivyofanya katika muji wa Adamu; kule walikosa uaminifu kwangu. Gileadi ni muji wa waovu, umejaa damu. Kama vile wanyanganyi wanavyomuvizia mutu katika njia, ndivyo makuhani walivyojikusanya na kuvizia. Wanaua watu katika njia yenye kuelekea Sekemu, na kutenda uovu mukubwa. Nimeona jambo la kuchukiza sana kati ya Waisraeli: watu wa Efuraimu wanakimbilia miungu mingine, Waisraeli wamejichafua. Nawe Yuda vilevile, nimekupangia wakati utakapovuna azabu. Kila mara nikitaka kurudishia watu wangu hali yao ya mbele, ninapotaka kuwaponyesha Waisraeli, uovu wa watu wa Efuraimu unafunuliwa, matendo mabaya ya Samaria yanajitokeza. Wao wanaongozwa na udanganyifu, mwizi anabomoa nyumba; inje katika barabara wanyanganyi wanashambulia. Hawafikiri hata kidogo kwamba mimi ninayakumbuka maovu yao yote. Sasa maovu yao yamewabana. Yote waliyotenda yako mbele yangu. Wanamufurahisha mufalme, lakini ni waovu; wanawafurahisha wakubwa, lakini ni wanafiki. Wote ni wazinzi; wao ni kama furu iliyowashwa moto ambayo mutengenezaji wa mikate haichochei tangia wakati anapoponda unga mpaka mikate itakapovimba. Kwenye sikukuu ya mufalme, waliwalewesha sana wakubwa wake; naye mufalme akashirikiana na watu wa ovyoovyo. Kama vile furu inavyowaka ndivyo mioyo yao inavyowaka kwa udanganyifu; usiku kucha hasira yao inafukiza moshi, inapofika asubui, inawaka kama ndimi za moto. Wote wamewaka hasira kama furu, na wanawaangamiza watawala wao. Wafalme wao wote wameanguka, wala hakuna anayeniomba musaada. Efuraimu amechanganika na watu wa mataifa. Anaonekana kama mukate ambao haukugeuzwa. Wageni wamenyonya nguvu zake, wala yeye mwenyewe hajui; imvi zimejaa juu ya kichwa chake, lakini yeye mwenyewe hana habari. Kiburi cha Waisraeli kinawashuhudia wao wenyewe, hawanirudilii mimi Yawe, Mungu wao; wala hawanitafuti kwa ajili ya matukio hayo yote. Efuraimu ni kama njiwa mujinga asiyekuwa na akili; mara yuko Misri, mara Asuria kwa kuomba musaada. Watakapokwenda nitatandaza wavu wangu niwanase, nitawaangusha chini kama ndege toka katika anga; nitamwaazibu kufuatana na jinsi walivyotangaza kwa kusanyiko lao. Ole kwao kwa sababu wameniacha! Maangamizi yawapate, maana wameniasi. Nilitaka kuwakomboa, lakini wanasema uongo juu yangu. Wananililia, lakini si kwa moyo. Wanagaagaa na kujikatakata juu ya vitanda vyao, kusudi nisikilize maombi yao kwa kupata ngano na divai; lakini wanaendelea kuniasi. Mimi ndimi niliyeiimarisha mikono yao, lakini wanafikiri maovu juu yangu. Wanaigeukia miungu ya bure, wako kama upinde ulioregea. Waongozi wao watakufa kwa upanga, kwa sababu ya maneno yao ya kiburi. Kwa hiyo, watazarauliwa katika inchi ya Misri. Mupige baragumu! Adui anakuja kama tai kuishambulia nyumba ya Yawe, kwa sababu wamelivunja agano langu na kuiasi sheria yangu. Waisraeli wananililia wakisema: Mungu wetu, sisi tunakujua. Lakini Waisraeli wametupilia mambo mazuri. Kwa hiyo, sasa waadui watawafuatilia. Walijiwekea wafalme bila ruhusa yangu, walijichagulia wakubwa ambao sikuwatambua. Wamejitengenezea miungu ya feza na zahabu, jambo ambalo litawaangamiza. Enyi watu wa Samaria, ninaichukia sanamu yenu ya mwana-ngombe. Hasira yangu inawaka juu yenu. Mutaendelea kuwa na makosa mpaka wakati gani? Ile sanamu inatoka Israeli, ni fundi ndiye aliyeitengeneza. Yenyewe si Mungu hata kidogo. Kweli! Sanamu ya mwana-ngombe ya Samaria itavunjwavunjwa! Wanapanda upepo, watavuna zoruba! Mimea yao ya ngano inayokuwa katika mashamba haitatoa ngano yoyote. Na hata kama ikizaa, mazao yake yatakuliwa na wageni. Waisraeli wamemezwa, wanakuwa kati ya mataifa mengine, kama chombo kisichokuwa na faida yoyote. Wamekwenda kuomba musaada Asuria. Efuraimu ni punda wa pori anayetangatanga peke yake; Efuraimu amejilipia wapenzi wake. Wametafuta wapenzi kati ya watu wa mataifa, lakini mimi nitawakusanya. Na hapo watasikia uzito wa muzigo wa mufalme wa wakubwa. Watu wa Efuraimu wamejijengea mazabahu nyingi, na mazabahu hizo zimewazidishia zambi. Hata kama ningewaandikia sheria zangu mara nyingi, wao wangeziona kuwa kitu cha kigeni tu. Wanapenda kutoa sadaka za nyama, kwa kusudi la kula nyama yake; lakini mimi Yawe sipendezwi hata kidogo. Mimi ninayakumbuka makosa yao; nitawaazibu kwa ajili ya zambi zao; nitawarudisha katika utumwa kule Misri. Waisraeli wamemusahau Muumba wao, wakajijengea nyumba kubwa; watu wa Yuda wamejiongezea miji yenye kuzungukwa na kuta, lakini mimi nitatuma moto katika miji hiyo, na kuziteketeza kuta zao. Musifurahi enyi Waisraeli! Musishangilie kama watu wa mataifa mengine; maana, mumekuwa wazinzi kwa kumwacha Mungu wenu. Mumefurahia malipo ya uzinzi, kwa kila nafasi ya kupepetea ngano. Hawatapata chakula kutoka kiwanja cha kupepetea, hawatapata divai mupya kutoka kikamulio. Hawatakaa katika inchi ya Yawe. Watu wa Efuraimu watarudi katika utumwa kule Misri. Watakula vyakula vichafu kule Asuria. Hawatamutolea Yawe sadaka ya divai, wala hawatamufurahisha kwa sadaka zao. Chakula chao kitakuwa kama cha kilio, wote watakaokikula watajichafua. Kitakuwa chakula cha kuwashibisha tu, hakitafaa kuletwa katika nyumba kwa Yawe. Mutafanya nini katika sikukuu ile iliyopangwa, au katika karamu ya Yawe? Mutakapoyakimbia maangamizi ya inchi yenu, Misri itawakaribisha ninyi kwake, lakini makaburi yenu yanawangoja kule Memufisi. Michongoma itaota katika vyombo vyenu vya feza, miiba itajaa katika mahema yenu. Siku za azabu zimetimia, siku za kulipiza kisasi zimefika; Waisraeli lazima wautambue wakati huo! Ninyi munasema: Nabii ni mupumbafu; anayeongozwa na roho ni mwenda-wazimu. Munasema hivyo kwa sababu ya uovu wenu mukubwa, kwa sababu ya chuki yenu kali juu yake. Nabii ni mulinzi wa Waefuraimu kwa pahali pa Mungu; lakini, popote anapoenda anategewa mutego kama ndege. Hata katika nyumba ya Mungu wake anachukiwa. Ninyi mumezama katika uovu, kama ilivyokuwa kule Gibea. Mungu atayakumbuka makosa yao, na kuwaazibu kwa ajili ya zambi zao. Yawe anasema: Nilipowakuta Waisraeli walikuwa kama zabibu katika jangwa. Nilipowaona babu zenu, walikuwa bora kama matunda ya tini za kwanza. Lakini walipofika kule Bali-Peori, wakajitolea kwa kuabudu chukizo Bali, wakakuwa chukizo kama kile walichokipenda. Utukufu wa Efuraimu utatoweka kama ndege; watoto hawatazaliwa tena, hakutakuwa watoto wa kuzaliwa, wala hakutakuwa atakayepata mimba! Hata kama wakilea watoto, sitamwacha hata mumoja wao muzima. Ole kwao, nitakapowaacha peke yao! Zamani, niliona kwamba Efuraimu ilikuwa kama muti wa ngazi muchanga kwenye nafasi nzuri. Lakini sasa Efuraimu italazimishwa kuwapeleka watoto wake wauawe. Uwaazibu watu hawa, ee Yawe! Lakini utawaazibu namna gani? Uwafanye wanawake wao kuwa tasa; uwafanye wakose maziwa ya kunyonyesha watoto wao! Yawe anasema hivi: Uovu wao wote ulianzia Gilgali; kule ndiko nilipoanza kuwachukia. Kwa sababu ya uovu wa matendo yao, nitawafukuza toka katika nyumba yangu. Sitawapenda tena. Wakubwa wao wote ni waasi. Watu wa Efuraimu wamepigwa, wamekuwa kama muti wenye muzizi wenye kukauka, hawatazaa watoto wowote. Hata kama wakizaa watoto, nitawaua watoto wao wanaowapenda. Kwa vile wamekataa kumusikiliza, Mungu wangu atawatupilia; wao watatangatanga kati ya mataifa. Waisraeli walikuwa kama muzabibu muzuri, muzabibu wenye kuzaa matunda. Kadiri matunda yalivyozidi kuongezeka, ndivyo walivyozidi kujijengea mazabahu. Kadiri inchi yao ilivyozidi kustawi, ndivyo walivyozidi kupamba nguzo zao za ibada. Mioyo yao imejaa udanganyifu. Sasa ni lazima wabebe makosa yao. Yawe atabomoa mazabahu zao na kuziharibu nguzo zao. Wakati huo watasema: Hatuna tena mufalme, kwa maana hatumwogopi Yawe; lakini, naye mufalme atatufanyia nini? Wanachosema ni maneno matupu; wanaapa na kufanya mapatano ya bure; haki imekuwa si haki tena, inachipuka kama mimea yenye sumu katika shamba. Wakaaji wa Samaria watatetemeka kwa sababu ya sanamu ya mwana-ngombe wa kule Beteli. Watu wake watamwombolezea mwana-ngombe yule, hata makuhani wanaomwabudu watamulilia; maana utukufu wa mwana-ngombe yule umeondolewa. Sanamu hiyo itapelekwa Asuria, kama zawadi kwa mufalme mukubwa. Watu wa Efuraimu watafezeheka, Waisraeli watapata haya kwa ajili ya sanamu yao. Mufalme wa Samaria atapelekwa, kama kipande cha muti juu ya maji. Pahali pa kutambikia juu ya vilima pa Aweni, pahali Waisraeli walipofanyia zambi, pataharibiwa. Miiba na michongoma vitaota katika mazabahu zao. Nao wataiambia milima: Mutufunike na vilima: Mutuangukie! Enyi Waisraeli, ninyi mumetenda zambi tangia kule Gibea, na mpaka sasa munaendelea. Hakika vita itawaangamizia kulekule Gibea. Nitawaendea watu hawa wapotovu na kuwaazibu; watu wa mataifa watakusanyika kwa kuwashambulia, watakapoazibiwa kwa ajili ya zambi zao nyingi. Efuraimu ni mwana-ngombe aliyefundishwa vizuri, akapenda kupepeta ngano. Lakini sasa shingo yake nzuri nitaifunga nira. Yuda atalima kwa jembe yeye mwenyewe, Yakobo atakokota jembe la kupalilia. Mupande haki kwa faida yenu, nanyi mutavuna wema; mulime mashamba yaliyoachwa, maana wakati wa kutafuta Yawe umefika kusudi awanyeshee haki kama mvua. Lakini ninyi mumepanda uovu, ninyi mumevuna ubaya; mumekula matunda ya uongo wenu. Wewe Israeli ulitegemea nguvu zako mwenyewe, na wingi wa waaskari wako. Kwa hiyo fujo ya vita itawafikia watu wako, kuta zako zote zitaharibiwa. Kama vile mufalme Salmani alivyoharibu Beti-Arbeli katika vita, wamama wakapondwa pamoja na watoto wao. Ndivyo itakavyokuwa kwenu enyi watu wa Beteli, kwa sababu ya uovu wenu mukubwa. Kutakapopambazuka mufalme wa Israeli atauawa. Israeli alipokuwa mutoto, nilimupenda. Kutoka Misri nilimwita mwana wangu. Lakini kadiri nilivyozidi kuwaita, ndivyo walivyozidi kwenda mbali nami; waliendelea kuyatambikia Mabali, na kuvifukizia ubani sanamu za miungu. Mimi ndiye niliyemufundisha watu wa Efuraimu kutembea! Mimi mwenyewe niliwatwaa katika mikono yangu; lakini hawakutambua kwamba mimi ndiye niliyewatunza. Niliwaongoza kwa huruma, nilishikamana nao kwa upendo; kama baba anavyomunyanyua mutoto mpaka kwenye shavu lake, ndivyo nami nilivyokuwa kwao. Mimi niliinama chini na kuwakulisha. Basi, watarudi katika inchi ya Misri; watatawaliwa na mufalme wa Asuria, kwa sababu wamekataa kunirudilia. Upanga utavuma katika miji yao, utavunjavunja miimo ya milango yake na kuwaangamiza katika kuta zao. Watu wangu wamekusudia kuniacha mimi, wakiitwa kusimama wapande juu, hakuna hata mumoja anayeweza. Ewe Efuraimu, ninaweza kukuacha namna gani? Ninaweza kukutupilia, ewe Israeli namna gani? Nitaweza namna gani kukufanya kama muji wa Adama? Nitaweza namna gani kukutendea kama Zeboimu! Ninazuizwa na moyo wangu; huruma yangu imezidi kuwa motomoto. Nitaizuia hasira yangu kali; sitamwangamiza tena Efuraimu, maana mimi ni Mungu, wala si mwanadamu. Mimi ndimi Mutakatifu kati yenu, nami sitakuja kuwaangamiza. Watanifuata mimi Yawe ninayenguruma kama simba; nitakaponguruma watanifikia toka magaribi wakitetemeka. Watakuja kutoka Misri wakitetemeka kama ndege, wataruka kutoka Asuria kama njiwa nami nitawarudisha kwao. –Ni ujumbe wa Yawe. Watu wa Efuraimu wananizunguka kwa uongo, na Waisraeli kwa udanganyifu. Lakini watu wa Yuda wanaendelea kuwa mwaminifu kwa Mungu Mutakatifu. Watu wa Efuraimu wanachunga upepo, muchana kutwa wanafukuza upepo wa mashariki. Wanazidisha uongo na mateso, wanafanya mapatano na Asuria na kupeleka mafuta Misri. Yawe ana mashitaki juu ya Yuda; atawaazibu wazao wa Yakobo kadiri ya makosa yao, na kuwalipa kadiri ya matendo yao. Yakobo akiwa angali katika tumbo la mama yake, alimushika kaka yake kisigino. Na alipokuwa mutu muzima alishindana na Mungu. Alipigana na malaika, akamushinda; alilia machozi na kuomba ahurumiwe. Kule Beteli, alikutana na Mungu, na kusemezana naye, Yawe wa majeshi, Yawe, ndilo jina lake. Lakini ninyi mumurudilie Mungu wenu. Mushikamane na wema na haki, mumutumainie Mungu wenu siku zote. Efuraimu ni sawa na muchuuzi anayetumia vipimo vya udanganyifu, anayependa kudanganya watu. Efuraimu amesema: Mimi ni tajiri! Mimi nimejitajirisha! Sikufanya mabaya kwa kupata hii faida. Yawe anasema: Mimi ni Yawe, Mungu wako, tangia katika inchi ya Misri! Mimi nitakukalisha tena katika mahema, kama vile mulivyofanya wakati nilipokutana nanyi. Mimi niliongea na manabii; ni mimi niliyewapa maono mengi, na kwa njia yao nilitangaza mupango wangu. Watu wa Gileadi walikuwa waovu sana; hakuna tena kitu kinachokuwa chao. Kule Gilgali walitambikia ngombe dume. Hivyo, mazabahu zao zitakuwa malundo ya mawe yaliyowekwa kwa mafungu katika shamba. Yakobo alikimbilia katika inchi ya Aramu. Akiwa huko alifanya kazi kusudi apate mwanamuke, akachunga kondoo kusudi apate mwanamuke. Kwa njia ya nabii, Yawe aliwatoa Waisraeli katika inchi ya Misri. Kwa njia ya nabii, Mungu aliwalinda. Waefuraimu wamemuchukiza Yawe sana. Lakini Yawe atawalipiza makosa yao, atawaazibu kwa mambo maovu waliyotenda. Waefuraimu waliposema, watu wote walitetemeka; Waefuraimu walikuwa na uwezo mukubwa katika inchi ya Israeli, lakini walianza kumwabudu mungu Bali, wakajiletea kifo. Waefuraimu wanaendelea kutenda zambi, wanajitengenezea sanamu za feza yenye kuyeyushwa, sanamu zinazotengenezwa kwa ufundi wao, zote zikiwa kazi ya wafundi. Wanasema: Muzitambikie! Wanaume wanabusu sanamu ya mwana-ngombe! Basi, watatoweka kama ukungu wa asubui, kama umande unaotoweka upesi; kama makapi yanayopeperushwa kwenye nafasi ya kupepetea, kama moshi unaotoka katika munara wa kutoshea moshi inje. Yawe anasema: Lakini mimi ni Yawe, Mungu wenu, niliyewatoa katika inchi ya Misri; hakuna mungu mwingine lakini mimi, wala hakuna anayeweza kuwaokoa. Ni mimi niliyewachunga mulipokuwa katika jangwa, katika inchi iliyokuwa yenye kukauka. Lakini mulipokwisha kula na kushiba, mulianza kuwa na kiburi, mpaka mukanisahau. Basi, nitakuwa kama simba kwenu ninyi wote; nitawavizia kama chui katika njia. Nitawarukia kama dubu aliyenyanganywa watoto wake. Nitawararua vifua vyenu na kuwakula palepale kama simba; nitawararua vipandevipande kama nyama wa pori. Nitawaangamiza, enyi Waisraeli. Nani ataweza kuwasaidia? Yuko wapi sasa mufalme wenu awaokoe? Wako wapi wale wakubwa wenu wawalinde? Ninyi ndio mulioomba: Utupatie mufalme na wakubwa watutawale. Kwa hasira yangu mimi nikawapa mufalme, kisha nikamwondoa kwa kasirani yangu. Uovu wa Efuraimu uko umeandikwa, zambi yake imewekwa akiba. Maumivu kama ya kuzaa mutoto yanamufikia. Lakini yeye ni mutoto mupumbafu; wakati wa kuzaliwa unapofika yeye anakataa kutoka ndani ya tumbo la mama! Inanipasa kuwakomboa hawa watu kutoka kuzimu; sharti niwaokoe kutoka kifo! Ewe kifo, mapigo yako ni wapi? Ewe kuzimu, kuangamiza kwako ni wapi? Mimi sitawaonea tena huruma! Hata kama Efuraimu atastawi kama nyasi, mimi Yawe nitavumisha upepo mukali wa mashariki, upepo utakaotokea kule katika jangwa, nao utakausha visima vyake, chemichemi zake zitakauka. Vitu vyake vyote vya bei kali vitaharibiwa. Watu wa Samaria wataazibiwa kwa ajili ya kosa lao; wamemwasi Mungu wao. Watauawa kwa upanga, watoto wao watapondwapondwa, na wamama wenye mimba watapasuliwa tumbo. Enyi Waisraeli, mumurudilie Yawe, Mungu wenu. Mumejikwaa kwa sababu ya uovu wenu. Muombe huruma kwake, mumurudilie na kumwambia: Utusamehe uovu wote, upokee zawadi zetu, nasi tutakusifu kwa moyo. Inchi ya Asuria haitatuokoa, hatutategemea tena farasi wa vita. Hatutaziita tena Mungu wetu hizo sanamu tulizochonga. Kwako, ee Mungu, yatima anapata huruma. Yawe anasema: Nitaponyesha ukosefu wao wa uaminifu; nitawapenda tena kwa moyo wangu wote, maana sitawakasirikia tena. Nitakuwa kama umande kwa Waisraeli nao watachanua kama mayungiyungi, watakuwa na mizizi kama muti wa mwerezi wa Lebanoni. Vichipukizi vyao vitazaa sana, uzuri wao utakuwa kama mizeituni, harufu yao nzuri kama maua ya Lebanoni. Watarudi na kuishi chini ya ulinzi wangu, watastawi kama bustani nzuri. Watachanua kama muzabibu, harufu yao nzuri kama ya divai ya Lebanoni. Enyi watu wa Efuraimu, muko na maneno gani tena na sanamu? Mimi ndiye ninayesikiliza maombi yenu, mimi ndiye ninayewatunza. Mimi nitawapa kivuli kama cha muti wa muberoshi; kutoka kwangu mutapata matunda yenu. Yeyote anayekuwa na hekima aelewe mambo haya, mutu anayekuwa na akili ayatambue. Maana njia za Yawe ni zenye kunyooka; watu wa haki wanazifuata, lakini wenye zambi wanaanguka katika njia hizo. Hili ni neno la Yawe lililomufikia Yoeli mwana wa Petueli. Musikilize kitu hiki, enyi wazee; mutege sikio, ninyi wakaaji wote wa Yuda! Jambo kama hili limekwisha kutokea katika maisha yenu, au nyakati za babu zenu? Muwaelezee watoto wenu jambo hili, nao wawaelezee watoto wao, na watoto wao wakielezee kizazi kinachofuata. Nzige, makundi kwa makundi, wameishambulia mimea; kilichoachwa na nzige kimekuliwa na tunutu, kilichoachwa na tunutu kimekuliwa na parare, kilichoachwa na parare kimeliwa na panzi. Enyi walevi, muamuke na kulia; enyi walevi wa divai, mulalamike; zabibu zote za kutengeneza divai mupya zimeharibiwa. Jeshi la nzige limeishambulia inchi yetu; lina nguvu na ni kubwa ajabu; meno yake ni kama ya simba, na mataya yake ni kama ya simba dike. Limeiharibu mizabibu yetu, na kuitafuna mitini yetu. Limeyabandua maganda yake na kuyatupa chini, na matawi yake yameachwa meupe. Mulie kama vile binti aliyevaa gunia akiombolezea kifo cha muchumba wake. Sadaka za vyakula na za kinywaji zimetoweka katika nyumba ya Yawe. Makuhani, watumishi wa Yawe, wanaomboleza. Mashamba yamebaki matupu. Inchi inaomboleza, maana ngano imeharibiwa, divai imetoweka, mafuta yamekosekana. Muomboleze, enyi walimaji; mulalamike, enyi watunza mizabibu. Ngano na shayiri zimeharibika, mavuno yote katika shamba yameangamia. Mizabibu imenyauka, mitini imekauka, miti yote ya matunda imekauka. Furaha imetoweka kati ya watu. Enyi makuhani, muvae magunia kwa kuomboleza, mulie, enyi munaotumika kwenye mazabahu. Muingie katika hekalu muomboleze usiku kucha! Sadaka za chakula na kinywaji zimetoweka katika nyumba ya Mungu. Mutoe amri watu wafunge kula chakula; muwaalike watu kuja kwa mukutano wa kidini. Mukusanye wazee na wakaaji wote wa inchi, katika nyumba ya Yawe, Mungu wenu, na mule mumulilie Yawe. Ole kwetu kwa ile siku ya Yawe, siku hiyo ya Yawe inakaribia; inakuja pamoja na maangamizi, kutoka kwa Mungu Mukubwa. Mazao yetu yameharibiwa mbele ya macho yetu. Furaha na kicheko vimetoweka katika nyumba ya Mungu wetu. Mbegu zinaoza ndani ya udongo; gala zimebaki bila kitu, vibanda vya kuwekea mavuno vimebomoka, kwa maana hakuna tena ngano. Angalia jinsi nyama wanavyolia kwa huzuni! Makundi ya ngombe yanahangaika, kwa sababu yamekosa malisho; hata makundi ya kondoo yanateswa. Ninakulilia wewe, ee Yawe, moto umemaliza malisho katika mbuga, ndimi za moto zimeteketeza miti katika mashamba. Hata nyama wa pori wanakulilia wewe, maana, vijito vya maji vimekauka, moto umemaliza malisho katika mbuga. Mupige baragumu kule Sayuni; mupige kelele la kujulisha hatari kule juu ya mulima mutakatifu! Mutetemeke enyi wakaaji wa Yuda, maana siku ya Yawe inakuja, siku hiyo iko karibu! Hiyo ni siku ya giza na huzuni; siku ya mawingu na giza nene. Jeshi kubwa linakaribia kama giza linalofunikia milima. Namna hiyo haijapata kuwa hata kidogo wala haitaonekana tena katika vizazi vyote vinavyokuja. Kama vile moto unavyoteketeza, Jeshi hilo linaharibu kila kitu mbele yake na kuacha nyuma kila kitu kinateketezwa; mbele ya kupita kwao, inchi ni kama bustani ya Edeni, lakini wakisha kupita, ni jangwa tupu. Hakuna kinachoweza kuponyoka! Wanaonekana kama farasi, wanashambulia kama farasi wa vita. Wanaporukaruka kwenye vilele vya milima, wananguruma kama magari yenye kukokotwa na farasi, wanavuma kama moto wa majani yenye kukauka. Wamejipanga kama kundi kubwa la waaskari tayari kabisa kufanya vita. Wanapokaribia, watu wanajaa hofu, nyuso zao zinawaivya. Wanashambulia kama mashujaa wa vita; wanapanda juu ya kuta kama waaskari. Wote wanakwenda mbele moja kwa moja, bila hata mumoja wao kubadilisha njia. Hakuna anayemusukuma mwenzake; kila mumoja anafuata njia yake. Wanapita kati ya vizuizi vya silaha, wala hakuna kinachoweza kuwazuia. Wanashambulia muji, wanakimbia juu ya ukuta; wanapanda juu ya nyumba na kuingia, wanapenya katika madirisha kama wezi. Inchi inatetemeka mbele yao, mbingu zinatikisika. Jua na mwezi vinatiwa giza, nazo nyota zinaacha kuangaza. Yawe anaamuru kundi lake kwa sauti; waaskari wake ni wengi sana, wanaomutii hawahesabiki. Siku ya Yawe kweli ni kubwa na ya kutisha sana! Nani atakayeweza kuivumilia? Lakini hata sasa, munirudilie kwa moyo wote, kwa kufunga kula, kwa kulia na kuomboleza. –Ni ujumbe wa Yawe.– Munapasua nguo zenu kwa kuonyesha huzuni, lakini inafaa mioyo yenu ipasuke vilevile. Murudilie Yawe, Mungu wenu. Yeye amejaa huruma na rehema, hakasiriki upesi, ni mwingi wa wema, na tayari kubadilisha nia zake kusudi asiazibu. Labda Yawe, Mungu wenu, atabadilisha nia na kuwapa baraka ya mazao, mutaweza kumutolea sadaka za chakula na kinywaji. Mupige baragumu kule Sayuni! Mutoe amri watu wafunge kula; muwaalike kuja kwa mukutano wa kidini. Muwakusanye watu wote, muwatakase watu. Muwalete wazee, muwakusanye watoto, hata watoto wanaonyonya. Bwana-arusi na bibi-arusi watoke katika vyumba vyao. Kati ya mazabahu na mulango wa hekalu, makuhani wanaomutumikia Yawe, walie na kuomba wakisema: Uwahurumie watu wako, ee Yawe. Usiyaache mataifa mengine yatuzarau na kutuchekelea yakisema: Yuko wapi basi Mungu wao? Yawe anaipenda inchi yake anawahurumia watu wake. Alisikiliza, akajibu maombi yao, akasema: Sasa nitawapa tena ngano, divai na mafuta, nanyi mutashiba navyo. Sitawafanya muzarauliwe tena na mataifa. Nitawaondoa hao waadui wanaotoka kaskazini, nitawafukuza mpaka katika jangwa; waaskari wa mbele nitawatupa katika bahari ya Chumvi na wale wa nyuma katika bahari ya Mediteranea. Watatoa uvundo na harufu mbaya, hao ambao wamefanya maovu makubwa. Usiogope, ewe inchi, lakini ufurahi na kushangilia, maana Yawe ametenda mambo makubwa. Musiogope, enyi nyama, malisho katika mbuga yamekuwa mazuri, miti inazaa matunda yake, mizabibu na mitini zinazaa kwa wingi. Mufurahi, enyi watu wa Sayuni, mushangilie kwa sababu ya Yawe, Mungu wenu, maana amewapa mvua zinazowafalia, amewapa mvua ya kutosha: mvua za kwanza na mvua za katikati kama pale mbele. Nafasi ya kupepetea itajaa ngano, vikamulio vitafurika divai na mafuta. Nitawarudishia miaka ile iliyokuliwa na nzige, kila kitu kilichokuliwa na tunutu, parare na panzi, hilo kundi kubwa nililowaletea! Mutapata chakula kingi na kutosheka; mutalisifu jina la Yawe, Mungu wenu, aliyewatendea mambo ya ajabu. Watu wangu, hawatazarauliwa tena hata kidogo. Mutatambua kwamba mimi niko kati yenu, enyi Waisraeli; na kwamba mimi Yawe, ndimi Mungu wenu wala hakuna mwingine. Watu wangu, hawatazarauliwa tena hata kidogo. Kisha mambo hayo nitashusha Roho wangu juu ya watu wote. Watoto wenu wanaume na wabinti watatabiri, wazee wenu wataota ndoto, na vijana wenu wataona maono. Hata juu ya watumishi wanaume na wanawake, nitashusha Roho wangu wakati huo. Nitafanya kitambulisho cha ajabu mbinguni na katika dunia; kutakuwa damu, moto na minara ya moshi. Jua litatiwa giza, na mwezi utakuwa kama damu, mbele ya kutimia kwa siku ya Yawe, siku inayokuwa kubwa na ya kutisha. Halafu, watu wote watakaoomba kwa jina la Yawe wataokolewa. Katika mulima Sayuni na Yerusalema, kutakuwa watu watakaoponyoka, kama vile Yawe alivyosema: wale aliowachagua watabaki wazima. Haya ni maneno ya Amosi, mumoja wa wachungaji wa nyama wa muji wa Tekoa. Mungu alimufunulia Amosi mambo haya yote juu ya inchi ya Israeli miaka miwili mbele ya tetemeko la inchi, wakati Uzia alipokuwa mufalme wa Yuda, na Yeroboamu mwana wa Yoasi alipokuwa mufalme wa Israeli. Amosi alisema hivi: Yawe ananguruma toka mulima Sayuni, anavumisha sauti yake toka Yerusalema, hata mashamba ya malisho ya wachungaji yanakauka, majani ya mulima Karmeli yananyauka. Yawe anasema hivi: Kwa sababu ya makosa matatu ya watu wa Damasiki, hata kwa mane, sitageuza nia yangu. Wamekatakata watu wa Gileadi wakitumia majembe ya mashini ya kulima. Basi, nitashusha moto juu ya nyumba ya mufalme Hazaeli, na kuziteketeza kabisa nyumba nzuri za mufalme Beni-Hadadi. Nitavivunjavunja vifungio vya milango ya muji wa Damasiki, na kuwaondoa wakaaji wa bonde la Aweni, pamoja na mutawala wa Beti-Edeni. Waaramu wanapelekwa katika uhamisho kule Kiri. –Ni Yawe anayesema hivyo. Yawe anasema hivi: Kwa sababu ya makosa matatu ya watu wa Gaza, hata kwa mane, sitageuza nia yangu. Wamekamata watu wengi na kuwapeleka kwa Waedomu. Basi, nitashusha moto juu ya kuta za muji wa Gaza, na kuziteketeza kabisa nyumba zake nzuri. Nitaondoa wakaaji wa muji wa Asidodi, pamoja na mutawala wa Asikeloni. Nitanyoosha mukono wangu kwa kuazibu muji wa Ekuroni, na Wafilistini wote waliobaki wataangamia. Ni mimi Yawe ninayesema hivyo. Yawe anasema hivi: Kwa sababu ya makosa matatu ya watu wa Tiro, hata kwa mane, sitageuza nia yangu. Wamekamata watu wengi na kuwapeleka mpaka Edomu. Hawakutii mapatano ya urafiki waliokuwa wamefanya. Basi, nitashusha moto juu ya kuta za muji wa Tiro, na kuziteketeza kabisa nyumba zake nzuri. Yawe anasema hivi: Kwa sababu ya makosa matatu ya watu wa Edomu, hata kwa mane, sitageuza nia yangu. Wamewawinda wandugu zao Waisraeli kwa mapanga, wakaitupilia mbali huruma yao yote ya kindugu. Hasira yao haikuwa na mwisho, waliiacha iwake siku zote. Basi, nitashusha moto juu ya muji wa Temani, na kuziteketeza kabisa nyumba nzuri za Bosira. Yawe anasema hivi: Kwa sababu ya makosa matatu ya watu wa Amoni, hata kwa mane, sitageuza nia yangu. Katika vita yao kwa kupanua inchi, walipasua tumbo za wanawake wenye mimba katika inchi ya Gileadi. Basi, nitashusha moto juu ya kuta za muji wa Raba, na kuziteketeza kabisa nyumba zake nzuri. Siku hiyo ya vita kutakuwa makelele mengi, nayo mapambano yatakuwa makali kama zoruba. Mufalme wao na wakubwa wake, wote watakwenda kukaa katika uhamisho. –Ni Yawe anayesema hivyo. Yawe anasema hivi: Kwa sababu ya makosa matatu ya watu wa Moabu, hata kwa mane, sitageuza nia yangu. Wamemukosea heshima marehemu mufalme wa Edomu kwa kuichoma mifupa yake kwa moto kwa kujitengenezea chokaa! Basi, nitashusha moto juu ya inchi ya Moabu, na kuziteketeza kabisa nyumba nzuri za muji wa Kerioti. Waaskari watakapolalamika kwa sauti zao na kupiga baragumu, watu wa Moabu watakufa katika makelele hayo ya vita. Nitamwua mutawala wa Moabu, pamoja na waongozi wote wa inchi hiyo. –Ni Yawe anayesema hivyo. Yawe anasema hivi: Kwa sababu ya makosa matatu ya watu wa Yuda, hata kwa mane, sitageuza nia yangu. Wamezarau sheria zangu, wala hawakufuata masharti yangu. Wamepotoshwa na miungu ileile babu zao waliyoifuata. Basi, nitashusha moto juu ya inchi ya Yuda, na kuziteketeza kabisa nyumba nzuri za Yerusalema. Yawe anasema hivi: Kwa sababu ya makosa matatu ya Waisraeli, hata kwa mane, sitageuza nia yangu. Wameuzisha watu wa haki kuwa watumwa kwa maana hawakuweza kulipa madeni yao; na kuwauzisha wakosefu wanaoshindwa kulipa deni la muguu mumoja wa mapapa. Wanagandamiza wazaifu, na kuwabagua wamasikini wasipate haki zao. Mutoto na baba yake wanalala na binti mujakazi mumoja, hivyo wanalichafua jina langu takatifu. Juu ya kila mazabahu, watu wanalalia nguo walizozitwaa kwa masikini kama rehani ya madeni yao; na katika nyumba ya Mungu wao, wanakunywa divai waliyotwaa kwa wenye kuwa na madeni yao. Hata hivyo, enyi watu wangu, kwa ajili yenu, niliwaangamiza kabisa Waamori ambao walikuwa wakubwa kama mierezi, wenye nguvu kama miti ya mialo. Niliwaangamiza, matawi na mizizi. Niliwatoa ninyi kutoka inchi ya Misri, nikawaongoza kupitia katika jangwa miaka makumi ine, mpaka mukaitwaa inchi ya Waamori kuwa yenu. Nilichagua manabii kati ya wana wenu, na wengine kati ya vijana wenu kuwa wanaziri. Enyi Waisraeli, haya ninayosema si ya kweli? –Ni ujumbe wa Yawe.– Ninyi muliwakunywesha wanaziri divai, na kuwaamuru manabii wasitoe unabii. Sasa basi, nitawagandamizia chini, kama gari lililojaa ngano. Hata wale wenye kuwa hodari kwa kukimbia mbio hawataweza kutoroka; wenye nguvu wataishiwa nguvu zao, na waaskari watashindwa kuyaokoa maisha yao. Wapiga upinde katika vita hawataweza kusimama na nguvu; wenye kuwa hodari kwa kukimbia mbio hawataweza kujiokoa, wala waaskari wapanda-farasi hawatayaokoa maisha yao. Siku hiyo, hata waaskari hodari sana watakimbia mbio bila chochote. –Ni ujumbe wa Yawe. Enyi Waisraeli, musikilize neno Yawe alilosema juu yenu, enyi taifa zima alilolitoa katika inchi ya Misri: Kati ya mataifa yote katika ulimwengu, ni ninyi tu niliowachagua. Kwa hiyo nitawaazibu ninyi, kwa sababu ya uovu wenu wote. Watu wawili wanaweza kusafiri pamoja bila kupatana kwanza? Simba ananguruma katika pori kama hajapata nyama? Simba mukali ananguruma katika pango lake kama hajakamata kitu? Mutego bila chambo utamunasa ndege? Mutego unaweza kufyatuka bila kuguswa na kitu? Baragumu ya vita inalia katika muji bila kutia watu hofu? Muji unaweza kupatwa na hasara ambayo haikuletwa na Mungu? Hakika, Bwana wetu Yawe hafanyi kitu bila kuwafunulia watumishi wake manabii nia yake. Simba akinguruma, ni nani asiyeogopa? Bwana wetu Yawe akisema, ni nani atakataa kuutangaza ujumbe wake? Mutangaze katika nyumba nzuri kule Asidodi, na katika nyumba nzuri za inchi ya Misri: Mukusanyike kwenye milima inayoizunguka inchi ya Samaria, mujionee fujo kubwa na mateso yanayofanyika kule. Hawajui kabisa kutenda mambo yanayokuwa sawa! –Ni ujumbe wa Yawe.– Wamejaza nyumba zao nzuri na vitu vya wizi na mateso. Kwa hiyo, Bwana wetu Yawe anasema hivi: Waadui wataizunguka inchi yenu, wataharibu kuta zako, na kuziteka nyumba zao nzuri. Yawe, anasema hivi: Kama vile muchungaji anavyonyanganya toka katika kinywa cha simba miguu miwili tu au kipande cha sikio la kondoo, ndivyo watu wachache tu wa Israeli wanaoishi Samaria, ambao sasa wanalalia vitanda vizuri na matandiko ya hariri watakavyobaki. Musikilize, muwaonye wazao wa Yakobo. –Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe, Mungu wa majeshi.– Siku nitakapowaazibu Waisraeli kwa sababu ya makosa yao, nitayaharibu vilevile mazabahu ya muji wa Beteli. Nitazikata pembe za kila mazabahu na kuziangusha chini. Nitaziharibu nyumba zote katika muji na katika vijiji; nitazibomoa nyumba zilizopambwa kwa pembe za tembo, nyumba kubwakubwa zitaanguka. –Ni ujumbe wa Yawe. Musikilize neno hili, enyi wanawake munaokuwa kama ngombe wa Basani munaokuwa kule juu ya mulima wa Samaria. Ninyi munaowaonea wamasikini, munaowagandamiza wakosefu, na kuwaambia waume zenu: Mutuletee divai tukunywe! Musikilize ujumbe huu: Bwana wetu Yawe Mutakatifu ameapa: Siku zinakuja ambapo watu watawakokota kwa ndoana kubwa, kila mumoja wenu kama samaki kwenye ndoana. Mutakokotwa mpaka kwenye ukuta ulipobomolewa, na kutupwa inje. –Ni ujumbe wa Yawe. Enyi Waisraeli, muende basi kule Beteli na kuniasi! Muende Gilgali muongeze makosa yenu! Mutoe sadaka zenu kila asubui na zaka zenu kwa siku ya tatu. Mutoe sadaka ya shukrani ya mikate isiyotiwa chachu. Mutangaze popote kwamba mumetoa kwa mapenzi; maana ndivyo munavyopenda kufanya! –Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe.– Mimi niliwanyima chochote cha kutafuna, nikasababisha ukosefu wa chakula popote. Hata hivyo hamukunirudilia. –Ni ujumbe wa Yawe.– Tena niliwanyima mvua miezi mitatu tu mbele ya mavuno. Nilinyeshea mvua muji mumoja, na muji mwingine nikaunyima. Shamba moja lilipata mvua, na lingine halikupata, likakauka. Watu wa miji miwili au mitatu wakakimbilia katika muji mwingine, wapate maji, lakini hayakuwatoshelea. Hata hivyo hamukunirudilia. –Ni ujumbe wa Yawe.– Niliwapiga pigo la ukosefu wa maji na ukungu; nikakausha bustani na mashamba yenu ya mizabibu; nzige wakakula miti ya tini na mizeituni yenu. Hata hivyo hamukunirudilia. –Ni ujumbe wa Yawe.– Niliwaletea ugonjwa mukali kama ule nilioupelekea Misri. Niliwaua vijana wenu katika vita, nikatwaa farasi wenu wa vita. Maiti zilijaa katika kambi zenu, harufu yake mbaya ikajaa katika pua zenu. Hata hivyo hamukunirudilia. –Ni ujumbe wa Yawe.– Niliwaangusha wamoja kati yenu kwa maangamizi kama nilivyoangamiza Sodoma na Gomora. Wale waliobaki kati yenu, walikuwa kama kijiti kilichookolewa katika moto. Hata hivyo hamukunirudilia. –Ni ujumbe wa Yawe.– Kwa hiyo, enyi Waisraeli, nitawaazibu. Na kwa sababu nitafanya jambo lile, mujitayarishe kwa kutana na Mungu wenu! Mungu ndiye aliyeifanya milima, na kuumba upepo; ndiye anayemujulisha mwanadamu mawazo yake; ndiye anayegeuza muchana kuwa usiku, na kukanyaga vilele vya dunia. Yawe wa majeshi ndilo jina lake! Musikilize maombolezo yangu juu yenu, enyi Waisraeli: Umeanguka na hautainuka tena ewe binti Israeli! Umeachwa ukiwa katika inchi yako, hakuna hata mutu wa kukuinua. Maana Bwana wetu Yawe anasema: Itakuwa hivi: juu yenu ninyi Waisraeli: Watu elfu moja wanatoka katika muji kwenda kupigana lakini watarudia watu mia moja tu; wataondoka watu mia moja wa kijiji kimoja lakini watu kumi tu wataponyoka. Yawe anawaambia Waisraeli hivi: Munitafute mimi nanyi mutaishi! Lakini musinitafutie kule Beteli wala musiende Gilgali wala musivuke kwenda Beri-Seba. Maana wakaaji wa Gilgali, hakika watapelekwa katika uhamisho, na Beteli utaangamizwa! Mutafute Yawe, nanyi mutaishi! Kama sivyo, atawatokea wazao wa Yosefu kama moto; moto utawateketeza wakaaji wa Beteli na hakuna mutu atakayeweza kuuzimisha. Angalisho, enyi munaogeuza sheria kuwa uchungu, na kuona haki kuwa kama takataka! Huyo aliyezifanya nyota zinazoitwa Kilimia na Orioni, ambaye analigeuza giza nene kuwa muchana, na muchana kuwa usiku; yeye anayekusanya maji ya bahari na kuyamwanga juu ya inchi kavu, Yawe ndilo jina lake. Yeye ndiye anayewaangamiza wenye nguvu, na kuziharibu kuta zao zenye nguvu. Ninyi munawachukia wanaotetea haki na wenye kusema ukweli katika tribinali. Ninyi munawagandamiza wazaifu na kuwalipisha kodi ya ngano. Munajijengea nyumba za mawe ya kuchongwa, lakini ninyi hamutaishi humo; munalima bustani nzuri za mizabibu, lakini hamutakunywa divai yake. Maana mimi ninajua wingi wa makosa yenu na ukubwa wa zambi zenu; ninyi munawatesa watu wema, munapokea kituliro na kuzuia wakosefu wasipate haki katika tribinali. Basi, kutakuwa wakati mubaya ambao hata mwenye hekima atanyamaza. Mutafute kutenda mazuri wala si mabaya, kusudi ninyi mupate kuishi naye Yawe wa majeshi atakuwa pamoja nanyi kama vile munavyosema. Muchukie mabaya, mupende mazuri, na kudumisha sheria ya Mungu katika tribinali. Labda Yawe wa majeshi atawarehemu watu wa kabila la Yosefu waliobaki. Basi, Yawe, Mungu wa majeshi, Bwana wetu anasema hivi: Kutakuwa kilio kila nafasi katika barabara za muji; watu wataomboleza: Ole! Ole! Walimaji wataitwa kuja kuomboleza, na wafundi wa kuomboleza kuja kufanya kilio. Kutakuwa kilio katika mashamba yote ya mizabibu; maana nitapita kati yenu kwa kuwaazibu. Ni Yawe anayesema hivyo. Ole kwenu ninyi munaoingojea kwa hamu siku ya Yawe! Kwa nini munaitaka sana siku hiyo? Siku hiyo, itakuwa siku ya giza na si ya mwangaza! Mambo yatakuwa kama mutu aliyekimbia simba, halafu anakutana na dubu! Au kama mutu anayerudi kwa nyumba yake, na kutia mukono wake kwenye ukuta, na kuumwa na nyoka. Siku ya Yawe itakuwa giza, na si mwangaza; itakuwa giza kubwa bila mwangaza wowote. Yawe anasema hivi: Ninachukia na kuzarau sikukuu zenu; siifurahii mikutano yenu ya kidini. Hata mukinitolea sadaka zenu za kuteketezwa kwa moto na za vyakula, mimi sitakubali kuzipokea; na sadaka zenu za amani za nyama wanono mimi sitaziangalia kabisa. Muondoe mbele yangu kelele za nyimbo zenu! Sitaki kusikiliza muziki wa vinubi vyenu! Lakini muache haki itiririke kama maji, usawa ukuwe kama muto usiokauka. Enyi Waisraeli, wakati ule mulipokuwa kule katika jangwa kwa miaka makumi ine, muliniletea matoleo na sadaka hata mara moja? Mulibeba kama vile sasa sanamu za mungu wenu Sakuti mufalme wenu na sanamu za Kiuni mungu wenu wa nyota, vitu ambavyo mulijitengenezea wenyewe? Kwa hiyo nitawapeleka katika uhamisho, mbali kuliko Damasiki! –Ni Yawe anayesema, ambaye jina lake ni Mungu wa majeshi. Ole kwenu ninyi munaostarehe kule Sayuni, nanyi munaoishi katika usalama kwenye mulima Samaria! Ninyi munaonekana kuwa waongozi wa taifa kubwa, ambao Waisraeli wote wanawategemea. Muende Kalne, muangalie. Tokea kule muende mpaka katika ule muji mukubwa wa Hamati, kisha mutelemuke mpaka Gati kwa Wafilistini. Mutatambua kwamba ninyi si bora kuliko falme zile, hata kama eneo lao ni ndogo zaidi ya lenu. Ninyi munajaribu kuifukuza ile siku mbaya. Lakini munaukaribisha utawala wa mateso. Ole kwenu ninyi munaolalia juu ya vitanda vya pembe za tembo na kujinyoosha juu ya matandiko yao, mukikula nyama za wana-kondoo na wana-ngombe! Ninyi munapenda kuimba ovyo na sauti ya vinubi na kutunga ala mupya za muziki mukimwiga mufalme Daudi. Munakunywa divai katika mabakuli, na kujipakaa marasi mazuri kabisa. Lakini hamuhuzuniki hata kidogo juu ya kuangamia kwa wazao wa Yosefu. Kwa hiyo mutakuwa wa kwanza kwenda katika uhamisho, na karamu za wenye kustarehe zitatoweka. Bwana wetu Yawe ameapa kwa nafsi yake: Ninachukizwa sana na kiburi cha wazao wa Yakobo; tena ninachukia nyumba zao nzuri sana. –Ni ujumbe wa Yawe.– Muji wao na vyote vinavyokuwa ndani yake nitavipatia waadui zake. Kama wakibaki watu kumi katika nyumba moja, wote watakufa. Na mujomba wa yule aliyekufa atakapokuja kuitoa maiti inje aichome, akimwuliza yeyote atakayekuwa ndani pembeni ya nyumba: Kuna mutu mwingine pamoja nawe? Atajibiwa: Hakuna! Naye atamwambia: Nyamaza kimya! Tusilitaje hata jina la Yawe. Yawe anatoa amri, na nyumba kubwa inabomoka vipandevipande, na nyumba ndogo kusagikasagika. Farasi wanaweza kukimbia katika mawe makubwa? Watu wanaweza kulima bahari na ngombe? Lakini ninyi mumeigeuza sheria kuwa sumu, na tunda la haki kuwa uchungu. Ninyi munashangilia juu ya muji wa Bure na kusema mumeuteka muji wa Nguvu kwa nguvu zenu wenyewe. Enyi Waisraeli, kweli nitaleta taifa moja likuje kuwashambulia. –Ni ujumbe wa Yawe.– Nalo litawatesa ninyi kuanzia Hamati upande wa kaskazini, mpaka kwenye kijito cha Araba, upande wa kusini. Bwana wetu Yawe alinionyesha hivi: Yawe alikuwa anaumba nzige kundi zima, nyuma ya watu kumaliza kukata majani kwa ajili ya nyama wa mufalme. Wakati ule, majani yalikuwa ndio yanaanza kuchipuka tena. Niliwaona nzige hao wakikula na kumaliza kila jani katika inchi. Halafu nikasema: Ee Bwana wetu Yawe, ninakusihi utuhurumie! Wazao wa Yakobo wataweza kuishi namna gani? Wao ni wadogo sana! Basi, Bwana wetu Yawe akabadilisha nia yake, akasema: Halitatukia! Bwana wetu Yawe alinionyesha tena maono mengine: Bwana wetu Yawe akiuita moto wa hukumu wa kuwaazibu watu. Moto ule uliunguza vilindi vikubwa vya bahari, ukaanza kuiteketeza inchi kavu. Halafu nikasema: Ee Bwana wetu Yawe, ninakusihi uache kuazibu! Wazao wa Yakobo wataweza kuishi namna gani? Wao ni wadogo sana! Basi, Yawe akabadilisha nia yake, akasema: Hili vilevile halitatukia. Yawe alinionyesha tena maono mengine: Yawe alikuwa anasimama karibu na ukuta, akishika katika mukono wake uzi wenye timazi. Naye akaniuliza: Amosi, unaona nini? Nikamujibu: Ninaona timazi. Kisha Yawe akasema: Ninaweka timazi kati ya watu wangu Waisraeli. Sitavumilia tena maovu yao. Kule kwenye vilima ambapo wazao wa Isaka wanatambikia, kutafanywa kuwa uharibifu mutupu na mahekalu ya Waisraeli yatakuwa mabomoko. Nitaushambulia kwa vita ukoo wa mufalme Yeroboamu. Basi, Amazia kuhani wa muji wa Beteli, akamupelekea mufalme Yeroboamu wa Israeli habari hii: Amosi analeta fitina juu yako katika ufalme wa Israeli. Hotuba zake ni hatari kwa inchi hii. Anachosema ni hiki: Yeroboamu atakufa kwa upanga nao Waisraeli watapelekwa katika uhamisho, mbali kabisa na inchi yao. Kisha Amazia akamwambia Amosi: Sasa tumechoka nawe, ewe nabii! Uende! Urudie katika inchi ya Yuda, utoe unabii kule upate na chakula chako kulekule. Usitoe tena unabii hapa katika Beteli, kwa sababu hapa ni pahali ya ibada ya mufalme; ni hekalu la utawala huu. Amosi akamujibu Amazia: Mimi si nabii wa mushahara, wala si mumoja wa kikundi cha manabii. Mimi ni muchungaji na mulimaji wa miti ya mikuyu. Yawe alinitosha katika kazi yangu hiyo ya uchungaji, akaniamuru nikuje kuwaambia watu wake wa Israeli unabii. Nawe basi, ewe Amazia, sikiliza neno la Yawe: Wewe unaniambia nisitoe unabii juu ya Waisraeli, wala nisiseme neno lolote juu ya wazao wa Isaka. Kwa hiyo, Yawe anasema hivi: Muke wako atakuwa kahaba katika muji, na wana wako na wabinti zako watauawa katika vita. Inchi yako itagawanywa na kupewa wengine, nawe mwenyewe utakufia katika inchi inayohesabiwa kuwa chafu; nao Waisraeli hakika watapelekwa katika uhamisho, mbali kabisa na inchi yao. Bwana wetu Yawe alinionyesha maono mengine: Niliona kikapu kilichojaa matunda yenye kuivya. Naye Yawe akaniuliza: Amosi, unaona nini? Nami nikamujibu: Ninaona kikapu cha matunda yenye kuivya. Kisha Yawe akaniambia: Mwisho umewafikia watu wangu wa Israeli. Sitavumilia tena maovu yao. Siku hiyo, nyimbo za nyumba ya kifalme zitakuwa maombolezo. –Ni ujumbe wa Yawe.– Kutakuwa maiti nyingi, nazo zitatupwa fasi zote kimyakimya. Musikilize, enyi munaowagandamiza wakosefu na kuwaletea maangamizi wamasikini wa inchi. Munajisemesha ndani ya mioyo yenu: Sikukuu ya mwandamo wa mwezi itakwisha wakati gani kusudi tuanze tena kuuzisha vyakula vyetu? Siku ya Sabato itakwisha wakati gani kusudi tupate kuuzisha ngano yetu? Tutapunguza vipimo, tutapandisha bei, tutadanganya watu kwa mizani zisizokuwa sawa. Tutawanunua wamasikini kwa feza na wakosefu kwa bei ya muguu mumoja wa mapapa. Nasi tutauzisha machenga ya ngano. Yawe, utukufu wa Yakobo, ameapa: Hakika, sitayasahau matendo yao maovu. Kwa hiyo, dunia itatetemeka na kila mutu katika inchi atafanya kilio. Inchi yote itayumbayumba; itapanda na kushuka, kama vile maji ya muto Nili yanavyojaa na kupunguka! Siku hiyo, nitalifanya jua litue pa saa sita za muchana, na kuijaza inchi giza wakati wa muchana. –Ni ujumbe wa Yawe.– Nitazigeuza sikukuu zenu kuwa kilio, na nyimbo zenu za furaha kuwa maombolezo. Nitawavalisha ninyi wote magunia kwa huzuni na kunyoa vichwa vyenu upaa, kama kuomboleza kifo cha mutoto wa pekee. Na siku ya mwisho itakuwa ya uchungu mukubwa. Siku zinakuja ambapo nitaleta njaa katika inchi. –Ni ujumbe wa Yawe.– Lakini si njaa ya kukosa chakula wala kiu ya kukosa maji, lakini njaa ya kusikia maneno ya Yawe. Watu watatangatanga kutoka bahari hata bahari, kutoka upande wa kaskazini mpaka wa mashariki. Watakimbia huko na huko wakitafuta neno la Yawe, lakini hawatalipata. Siku hiyo, wabinti wazuri na vijana wanaume watazimia kwa kiu. Wale wanaoapa kwa mungu wa uongo wa Samaria na kusema “Kwa nafsi ya mungu wako ee Dani” au “Kwa nafsi ya mungu wa Beri-Seba”, wote wataanguka na hawatasimama tena hata kidogo. Nilimwona Yawe akisimama pembeni ya mazabahu, naye akaniamuru: Piga zile nguzo za hekalu mpaka misingi yake itikisike. Uvunje zile nguzo ziwaangukie watu juu ya vichwa. Wale watakaobaki nitawaua kwa upanga; hakuna hata mumoja wao atakayeponyoka, hakuna atakayetoroka. Hata wakijichimbia njia ya kwenda kuzimu, nitawakamata kule kwa mukono wangu; hata wakipanda juu mbinguni, nitawaporomosha chini. Hata wakijificha juu ya mulima Karmeli, huko nitawatafuta na kuwakamata; hata wakijificha mbali nami katika vilindi vya bahari, mule nitaiamuru nyoka kubwa ya bahari iwaume. Hata wakikamatwa mateka na waadui zao, nitatoa amri kule wauawe kwa upanga. Nitawachunga kwa uangalifu sana nipate kuwatendea mabaya na si mema. Bwana wetu Yawe wa majeshi, anaigusa dunia nayo inatetemeka, na wakaaji wake wanaomboleza; dunia nzima inapanda na kushuka kama vile muto Nili wa Misri unavyojaa na kupunguka. Yawe amejenga makao yake mbinguni, nayo dunia akaifunika kwa anga; anayaita maji ya bahari, na kuyamwanga juu ya inchi kavu. Yawe, ndilo jina lake! Kwangu mimi, ninyi Waisraeli, muko sawasawa na watu wa Kushi! –Ni ujumbe wa Yawe.– Niliwatoa Wafilistini kutoka Krete, na Waaramu kutoka Kiri, kama nilivyowatoa ninyi kutoka Misri. Ninauangalia ufalme wenye zambi, na nitauangamiza kabisa kutoka katika dunia. Lakini sitawaangamiza wazao wote wa Yakobo. –Ni ujumbe wa Yawe. Nitatoa amri, na kuwapepeta Waisraeli kati ya mataifa kama mutu anavyopepeta ngano kusudi niwatoshe wote wasiofaa. Wenye zambi kati ya watu wangu, watakufa katika vita. Hao ndio wanaosema: Hasara haitatufikia wala kutupata! Siku inakuja nitakapoisimika nyumba ya Daudi iliyoanguka; nitazitengeneza kuta zake, na kusimika upya mabomoko yake. Nitaijenga upya kama ilivyokuwa tangu zamani. Nao Waisraeli watarizi mabaki ya inchi ya Edomu na mataifa yote yaliyokuwa yangu. –Ni ujumbe wa Yawe, yule anayefanya hivyo. Siku zinakuja ambapo wakati wa kuvuna utafuata mbio wakati wa kulima, wakati wa kukamua zabibu utafuata mbio wakati wa kupanda mizabibu. –Ni ujumbe wa Yawe.– Milima itabubujika divai mupya, navyo vilima vitatiririka divai. Nitarudisha hali ya mbele ya watu wangu Waisraeli. Watajenga miji yao iliyoharibiwa na kuishi ndani yake; watapanda mizabibu na kunywa divai yake; watalima mashamba na kula mazao yake. Nitawasimika katika inchi yao, wala hawataongolewa tena kutoka katika inchi niliyowapa. –Ni Yawe anayesema hivyo. Haya ni maono ya Obadia. Bwana wetu Yawe anasema hivi juu ya taifa la Edomu. Tumepata habari kutoka kwa Yawe; mujumbe ametumwa kati ya mataifa: Musimame! Tuende tupigane na taifa la Edomu! Yawe aliambia taifa la Edomu: Nitakufanya kuwa mudogo kati ya mataifa, utazarauliwa kabisa na wote. Kiburi chako kimekudanganya: wewe unayekaa ndani ya mashimo chini ya mawe makubwa na makao yako yapo juu kwenye milima, hivyo unajisemesha: Nani anayeweza kunishusha chini? Hata ukiruka juu kama tai, ukifanya makao yako kati ya nyota, mimi nitakushusha chini tu. –Ni ujumbe wa Yawe. Kama wizi au wanyanganyi wangekufikia usiku, si wao wangekuiba tu vitu wanavyokuwa navyo lazima? Ikiwa wavunaji wa zabibu wangekufikia, si wangekuachia sehemu ndogo tu? Lakini wewe, waadui zako wamekuangamiza kabisa. Enyi wazao wa Esau, mali yenu imenyanganywa, akiba zenu zote zilizofichwa zimevumbuliwa! Washirika wenzenu wamewadanganya, wamewafukuza toka katika inchi yenu. Watu muliopatana nao wamewashinda katika vita. Warafiki wa kutegemewa ndio waliokutegea mitego, nawe haukuelewa yaliyokuwa yanatendeka. Mimi Yawe ninakuuliza hivi: Siku hiyo, sitawaangamiza wenye hekima kutoka Edomu na wenye maarifa kutoka mulima wa wazao wa Esau? Ewe muji wa Temani, mashujaa wako wataogopa na kila mutu juu ya mulima wa wazao wa Esau. Kwa sababu ya mateso makali muliyowatendea wandugu zenu wazao wa Yakobo, mutafezeheshwa na kuangamizwa milele. Siku ile mulisimama pembeni mukiangalia tu, wakati wageni walipouteka utajiri wao, walipoingia katika milango yake na kugawanya utajiri wa Yerusalema kwa kupiga kura. Nanyi vilevile mulikuwa kama wamoja wao. Hamukupaswa kuangalia tu siku hiyo wandugu zenu walipopatwa na taabu, hamukupaswa kufurahi juu ya Wayuda siku hiyo walipoangamizwa, hamukupaswa kujivuna siku ile wenzenu walipokuwa wanateseka, hamukupaswa kuingia katika muji wa watu wangu, siku walipopatwa na hasara, hamukupaswa kukamata mali zao, siku hiyo ya hasara yao, hamukupaswa kusimama kwenye masanganjia na kuwakamata wakimbizi wao, hamukupaswa kuwatoa kwa waadui zao wale waliobaki wazima. Siku inakaribia ambapo mimi Yawe nitayahukumu mataifa yote. Kama vile mulivyowatendea wengine, ndivyo mutakavyotendewa, mutalipwa kulingana na matendo yenu. Maana, kama walivyokunywa kikombe cha kasirani yangu kwenye mulima wangu mutakatifu, ndivyo mataifa jirani watakavyokunywa; watakunywa na kupepesuka, wataangamia na kuwa kama hawakukuwa mbele katika dunia. Lakini wale waliobaki watakaa kwa mulima Sayuni nao utakuwa mulima mutakatifu. Wazao wa Yakobo watanyanganya inchi yao toka kwa wale waliokuwa wameinyanganya. Wazao wa Yakobo watakuwa kama moto na wazao wa Yosefu kama ndimi za moto. Watawaangamiza wazao wa Esau kama vile moto unavyoteketeza majani yenye kukauka, hakutaponyoka hata mumoja wao. –Yawe amesema. Wale wanaokaa Negebu wataurizi mulima wa wazao wa Esau, wale wanaokaa katika Shefela watarizi inchi ya Wafilistini. Waisraeli watarizi inchi za Efuraimu na Samaria na watu wa kabila la Benjamina watarizi inchi ya Gileadi. Waisraeli wanaokuwa katika uhamisho, lile jeshi la Waisraeli, watarizi inchi ya Foinikia mpaka Zerepata. Watu wa Yerusalema wanaokuwa katika uhamisho kule Sefaradi watarizi miji ya Negebu. Wakombozi watapanda juu ya mulima Sayuni kwa kuutawala mulima wa wazao wa Esau; naye Yawe atakuwa ndiye Mufalme. Neno la Yawe lilimufikia Yona mwana wa Amitai kusema hivi: Simama, uende Ninawe, ule muji mukubwa, uukaripie. Maana uovu wake umenifikia. Basi, Yona akasimama kwa kukimbilia Tarsisi, mbali na uso wa Yawe. Akaenda mpaka katika muji wa Yofa ambapo alikuta mashua moja iko tayari kwenda Tarsisi. Alilipa bei ya safari, akapanda ndani ya mashua, akasafiri pamoja na watu wengine kwenda Tarsisi, mbali na uso wa Yawe. Lakini Yawe akavumisha upepo mukali katika bahari, kukatokea zoruba kali. Mashua ikakuwa karibu kuvunjika kabisa. Watumishi wa mashua wakaogopa, kila mumoja akaanza kumulilia mungu wake. Wakatupa katika bahari mizigo yote kwa kupunguza uzito wa mashua. Wakati ule, Yona alikuwa ameshuka katika sehemu ya ndani ya mashua, akalala usingizi muzito. Kapiteni wa mashua akamwendea, akamwambia: Namna gani wewe unaweza kulala? Amuka umwombe Mungu wako; labda Mungu wako atatuhurumia na kuyaokoa maisha yetu. Kisha wale watumishi wa mashua wakasemezana: Tupige kura tupate kujua hasara hii imetupata kwa ajili ya kosa la nani. Basi, wakapiga kura; kura ikamwangukia Yona. Kwa hiyo wakaanza kumwuliza: Sasa utuambie! Kwa nini hasara hii inatupata? Unafanya kazi gani? Umetoka wapi? Inchi yako ni gani? Uko wa kabila gani? Yona akawajibu: Mimi ni Mwebrania; ninamwabudu Yawe, Mungu wa mbingu, muumba wa bahari na inchi kavu. Kisha Yona akawaelezea kwamba alikuwa anamukimbia Yawe. Kusikia hayo, watu hao wakazidi kuogopa, wakamwambia: Kwa sababu gani umefanya vile? Wakati huo wote, bahari ilikuwa inazidi kuchafuka. Basi, wakamwuliza Yona: Tukufanye nini kusudi bahari itulie? Yona akawajibu: Munikamate na kunitupa katika bahari, nayo bahari itatulia, maana ninaona wazi kwamba zoruba hii imewapata kwa sababu yangu mimi. Watumishi wale wakajaribu kuvuta makasia wapate kuifikisha mashua yao inchi kavu, lakini hawakufanikiwa kwa maana bahari ilizidi kuwachafukia. Basi, wakamulilia Yawe wakisema: Ee Yawe, tunakusihi usituangamize kwa kuutoa uzima wa mutu huyu, wala usituazibu kwa kumwanga damu ya mutu asiyekuwa na kosa. Wewe, ee Yawe, umefanya unavyopenda. Basi, wakamukamata Yona, wakamutupa ndani ya bahari na palepale bahari ikatulia. Watu hao wakamwogopa sana Yawe, wakamutolea sadaka na kufanya viapo. Kisha, Yawe akaamuru samaki mukubwa amumeze Yona, naye akabaki ndani ya tumbo la samaki huyo kwa muda wa siku tatu, usiku na muchana. Basi, Yona akiwa ndani ya tumbo la samaki yule, akamwomba Yawe Mungu wake, akisema: Kwa sababu ya taabu yangu, nilikuomba, ee Yawe, nawe ukanisikiliza; toka chini kuzimu, nilikulilia, nawe ukasikiliza kilio changu. Ulinitupa katika kilindi, katikati ya bahari, maji mengi yakanizunguka, mawimbi na maji mengi vikapita juu yangu. Nilizani kwamba nimetupwa mbali nawe; nisiweze kuliona tena hekalu lako takatifu. Maji yalinizunguka na kunisonga; kilindi kilinifikia kila upande, majani ya bahari yakanifunika kichwa. Niliteremuka mpaka kwenye misingi ya milima, katika inchi ambayo milango yake imefungwa milele. Lakini wewe, ee Yawe, Mungu wangu, umenipandisha nikiwa muzima kutoka mule ndani ya shimo. Roho yangu ilipoanza kunitoka, nilikukumbuka, ee Yawe, maombi yangu yakakufikia katika hekalu lako takatifu. Watu wanaoabudu sanamu za miungu ya bure, wanautupilia mbali uaminifu wao kwako. Lakini mimi, kwa wimbo wa shukrani, nitakutolea sadaka, na kutimiza viapo vyangu. Yawe, ndiye anayeokoa. Basi, Yawe akamwamuru yule samaki, naye akamutapika Yona kwenye inchi kavu. Neno la Yawe lilimufikia Yona mara ya pili kusema hivi: Simama, uende Ninawe, ule muji mukubwa, uwatangazie watu ujumbe ninaokupa. Basi, Yona akaondoka, akaenda Ninawe kama vile Yawe alivyomwagiza. Muji wa Ninawe ulikuwa mukubwa sana. Upana wake ulikuwa mwendo wa siku tatu. Alipofika, Yona aliingia katika muji. Kisha kutembea mwendo wa siku nzima, akaanza kutangaza: Kunabaki siku makumi ine tu na muji huu wa Ninawe utaangamizwa! Basi, watu wa Ninawe wakauamini ujumbe wa Mungu, wakatangaza kufunga kula chakula, na kwamba kila mumoja wao, mukubwa kama vile mudogo, avae gunia. Habari hizi zikamufikia mufalme wa Ninawe, naye akaondoka juu ya kiti chake cha kifalme, akavua nguo yake ya kifalme, akavaa gunia na kuikaa katika majivu. Kisha mufalme akawatangazia wakaaji wa Ninawe: Mimi mufalme, pamoja na wakubwa wangu, ninatoa amri hii: Kusikuwe mutu yeyote, ngombe au nyama yeyote wa kufugwa, atakayeonja kitu chochote. Hairuhusiwi kwa mutu yeyote au nyama kula au kunywa. Watu wote na nyama wavae gunia. Kila mutu amwombe Mungu na kumusihi kwa moyo. Kila mumoja aache uovu wake, aache kutenda kwa ukali. Labda Mungu atabadilisha nia yake, na kuacha kutukasirikia, nasi hatutaangamizwa! Mungu alipoona walivyofanya, na jinsi walivyouacha uovu wao, akabadilisha nia yake, akaacha kuwatenda kama alivyokuwa amekusudia. Lakini jambo hilo halikumupendeza Yona hata kidogo, akakasirika sana. Kwa hiyo akaomba: Yawe, si hayo ndiyo mambo yaleyale niliyowaza utayafanya nilipokuwa katika inchi yangu? Ndiyo maana nilifanya haraka kukimbilia Tarsisi. Nilijua kwamba wewe ni Mungu ambaye umejaa huruma na rehema, haukasiriki upesi, wewe ni mwingi wa wema, na tayari kubadilisha nia yako kusudi usiazibu. Basi, sasa ee Yawe, ninakusihi uniondoe uzima wangu, maana ni vizuri kwangu kufa kuliko kuishi. Naye Yawe akamujibu Yona: Unazani kwamba unafanya vema kukasirika? Halafu Yona akatoka inje ya muji, akajiikalia upande wa mashariki wa muji huo. Pale, akajijengea kibanda, akaikaa chini ya kivuli chake akingojea apate kuona jambo litakaloupata muji wa Ninawe. Mungu, Yawe akaamuru mumea uote na kukomaa. Akauotesha kwa kumupatia Yona kivuli cha kumupunguzia taabu aliyokuwa nayo. Yona akaufurahia sana mumea huo. Lakini kesho yake kulipopambazuka, Mungu akaamuru mududu uharibu mumea huo. Ukanyauka. Jua lilipotokea, Mungu akaleta upepo mukali kutoka upande wa jangwa, jua likamuchoma sana Yona juu ya kichwa, karibu azimie. Akatamani kufa, akisema: Ni vizuri kwangu kufa kuliko kuishi. Lakini Mungu akamwuliza Yona: Unazani unafanya vema kuukasirikia mumea huo? Yona akajibu: Ndiyo, ninafanya vema kukasirika – kukasirika hata kufa! Basi Mungu akamwambia: Mumea huu uliota na kukomaa kwa usiku mumoja, na usiku uliofuata ukanyauka. Wewe haukuufanyia kitu chochote, wala haukuuotesha. Mbona unausikilia huruma? Basi, haifai kwangu kuuhurumia Ninawe, ule muji mukubwa wenye watu elfu mia moja na makumi mbili, wasioweza kutambua linalokuwa jema na baya; na nyama wengi wasiokuwa na hesabu? Hili ni neno la Yawe lilomufikia Mika, wa muji wa Moreseti wakati Yotamu, Ahazi na Hezekia walipokuwa wafalme wa Yuda. Mika aliona mambo yote haya juu ya Samaria na Yerusalema. Musikilize enyi watu wote; sikiliza ewe dunia na vyote vinavyokuwa ndani yako. Bwana wetu Yawe anakuja kuwashitaki, Bwana wetu anasema kutoka hekalu lake takatifu. Kweli, anakuja kutoka makao yake; atashuka na kutembea juu ya vilele vya dunia. Milima itayeyuka chini ya miguu yake, kama inta karibu na moto; mabonde yatapasuka, kama vile maji yanayoporomoka kwenye muteremuko. Haya yote yatatukia kwa sababu ya makosa ya wazao wa Yakobo, kwa sababu ya zambi za wazao wa Israeli. Kosa la Yakobo linaonekana wapi? Katika muji wake mukubwa Samaria! Kosa la Yuda linaonekana wapi? Katika Yerusalema kwenyewe! Kwa hiyo, anasema hivi: Muji wa Samaria nitaufanya kuwa mabomoko katika mbuga, shamba ambalo watu watapanda mizabibu. Mawe yaliyoujenga nitayatupa ndani ya bonde, na misingi yake nitaichimbuachimbua. Sanamu zake zote zitavunjwavunjwa, kila kitu kilichochumwa kitateketezwa kwa moto. Nitaharibu sanamu za miungu yake yote. Zililundikwa kutokana na mushahara wa ukahaba, nazo zitatumiwa tena kuwa mushahara wa ukahaba. Kwa sababu hiyo, mimi nitalia na kuomboleza; nitatembea uchi na bila viatu. Nitaomboleza na kulia kama mbweha, nitasikitika na kulia kama mbuni. Vidonda vya Samaria haviwezi kupona, navyo vimeipata vilevile inchi ya Yuda; vimefikia kwenye mulango wa Yerusalema, pahali watu wangu wanapokaa. Musiitangaze habari hii kule Gati, wala musilie machozi! Kule Beti-Leafura mugaegae katika mavumbi kwa huzuni. Enyi wakaaji wa Safiri, muende mukiwa uchi na wenye haya. Wakaaji wa Zanana musitoke inje ya muji wenu. Watu wa Beti-Ezeli wanalia; musaada wao kwenu umeondolewa. Wakaaji wa Maroti wanangojea musaada kwa hamu kubwa, lakini maangamizi yanakuja kutoka kwa Yawe karibu kabisa na mulango wa Yerusalema. Enyi wakaaji wa Lakisi, mufunge farasi wepesi na magari ya vita. Ninyi mulikuwa mumeiga zambi ya watu wa Sayuni, makosa ya Waisraeli yalikuwa kwenu. Hivyo, munapaswa kuwaacha wakaaji wa Moreseti-Gati. Nao muji wa Akizibu hautawasaidia wafalme wa Israeli kwa kitu chochote. Enyi wakaaji wa Maresa, Mungu atawaletea tena adui atakayewateka. Waongozi waheshimiwa wa Israeli watakimbilia ndani ya pango kule Adulamu. Enyi watu wa Yuda, munyoe vichwa vyenu kwa kuwaomboleza watoto wenu wapenzi; mupanue upaa wenu ukuwe mupana kama wa tai, maana watoto wenu watawaacha kwenda katika uhamisho. Ole wao wanaopanga kutenda maovu, wanaolala usiku wakikusudia mabaya! Mara tu kunapopambazuka, wanayatimiza maana wako na uwezo. Wanatamani mashamba na kuyatwaa; wakitaka nyumba, wananyanganya. Wanawatesa wenye nyumba na jamaa zao, wanawanyanganya watu mali zao. Kwa hiyo, Yawe anasema hivi: Ninapanga kuwaletea ninyi hasara, ambayo hamutaweza kuiponyoka hata kidogo. Utakuwa wakati mubaya kwenu, wala hamutaweza kutembea kwa maringo. Siku hiyo watu watawasimanga kwa wimbo, watalia na kuomboleza kwa uchungu, wakisema: Tumeangamia kabisa; amekamata inchi yetu, ameiondoa katika mikono yetu. Mashamba yetu ameyagawanya kwa wale waliotuteka. Kwa hiyo hamutagawanyiwa sehemu yoyote ya inchi kati ya watu wa Yawe. Usituhubirie sisi. Mambo kama hayo si ya kuhubiriwa. Sisi hatutapatwa na hasara! Inafaa kusema hivyo, enyi wazao wa Yakobo? Yawe ameacha uvumilivu wake? Yeye anafanya mambo kama haya? Maneno yangu yanawafalia wenye mwenendo sawa. Lakini Yawe anawaambia ninyi hivi: Munawatendea watu wangu kama adui. Munawanyanganya watu watulivu nguo zao; watu wanaopita kwenda zao bila wasiwasi, na wasiokuwa na mafikiri yoyote ya vita. Munawafukuza wake za watu wangu kutoka nyumba zao nzuri. Mumewaondolea watoto wao utukufu wangu milele. Musimame! Muende! Hapa hakuna tena pahali pa kupumzika! Kwa ajili ya ukosefu wenu wa uaminifu, maangamizi makubwa yanawangojea! Kama mutu angetokea akitangaza maneno matupu ya uongo na kusema “Ninawatabiria divai na pombe kwa wingi”, muhubiri wa namna hiyo angependwa na watu hawa! Lakini kweli nitawakusanya ninyi wote enyi watu wa Yakobo, nitawakusanya enyi Waisraeli muliobaki, niwalete pamoja kama kondoo katika zizi, kama kundi kubwa la kondoo katika shamba la malisho; nanyi mutakuwa kundi la watu wengi. Yule atakayepasua njia atawatangulia, nanyi mutauvunja mulango wa muji na kutoka inje, mutapita na kutoka inje. Mufalme wenu, atawatangulia; Yawe mwenyewe atawatangulia. Sasa musikilize, enyi wakubwa wa wazao wa Yakobo, musikilize, enyi watawala wa wazao wa Israeli! Ninyi ndio munaopaswa kujua namna ya kufuata sheria ya Mungu. Lakini ninyi munachukia mazuri na kupenda mabaya. Munawachuna ngozi watu wangu, na kunyofoa nyama juu ya mifupa yao. Munajikulisha kwa nyama ya watu wangu, munawachuna ngozi yao, munaivunjavunja mifupa yao, na kuwakatakata kama nyama ya kupika, kama nyama ya kutia ndani ya chungu. Wakati unakuja ambapo mutamulilia Yawe, lakini yeye hatawajibu. Atauficha uso wake wakati huo, kwa sababu mumetenda mambo maovu. Yawe anasema hivi juu ya manabii wanaowapotosha watu wake, manabii ambao wanatabiri amani wakipewa kitu, lakini wanawatishia watu kwa vita wasipopewa kitu: Kwenu manabii kutakuwa usiku bila maono, kutakuwa giza kwenu bila ufunuo. Jua litatua juu yenu, na muchana utakuwa giza kwenu. Waonaji watafezeheka, waaguzi watapata haya; wote watafunga midomo yao, maana hawatapata jibu lolote kutoka kwa Mungu. Lakini kwa upande wangu, nimejazwa nguvu na roho ya Yawe; nimejaliwa kufuata sheria ya Mungu na kuwa na uwezo niwatangazie wazao wa Yakobo kosa lao, niwaambie Waisraeli zambi yao. Musikie jambo hili, enyi waongozi wa wazao wa Yakobo, musikilize, enyi watawala wa Waisraeli: Ninyi munachukia sheria ya Mungu na kupotosha mambo ya usawa. Ninyi munajenga Sayuni kwa damu, Yerusalema kwa uovu. Waamuzi wanahukumu kwa kupewa kutuliro, makuhani wake wanafundisha kwa kupata malipo, manabii wanatabiri kwa kupata feza. Hata hivyo wanajidai kumutegemea Yawe, wakisema: Yawe, si yupo pamoja nasi? Hatutapatwa na hasara yoyote! Basi! Kwa sababu yenu, Sayuni utalimwa kama shamba, Yerusalema lundo la makokoto, nao mulima wa hekalu utakuwa pori. Kutakuja wakati ambapo mulima wa nyumba ya Yawe utakuwa mukubwa kuliko milima yote. Utanyanyuliwa juu ya vilima vyote. Watu wengi watakimbilia kule, mataifa mengi yataufikia na kusema: Tuende juu kwenye mulima wa Yawe, tuende katika nyumba ya Mungu wa Yakobo, kusudi atufundishe njia zake, nasi tuzifuate. Maana sheria itatoka kule Sayuni; na neno la Yawe kule Yerusalema. Mungu atatoa hukumu kati ya mataifa mengi, atakata mashauri ya mataifa makubwa ya mbali. Nayo yatafua mapanga yao kuwa majembe, na mikuki yao kuwa visu vya kuvuna. Taifa halitapigana na taifa lingine, wala hayatafanya tena mazoezi ya vita. Kila mutu atakaa kwa amani chini ya miti ya tini na mizabibu yake, bila kutishwa na mutu yeyote. –Maneno haya yanatoka katika kinywa cha Yawe wa majeshi. Mataifa mengine yanafuata njia zao, kwa kuitegemea miungu yao, lakini sisi tunafuata njia zetu kwa kumutegemea Yawe, Mungu wetu, milele na milele. Siku ile, nitawakusanya waliolemewa, nitawakusanya waliopelekwa katika uhamisho, watu wale ambao niliwaazibu. –Ni ujumbe wa Yawe.– Hao waliolemewa ndio watakaobaki wazima; hao waliopelekwa katika uhamisho watakuwa taifa lenye nguvu. Yawe atawatawala kwenye mulima Sayuni, tangu wakati ule na hata milele. Nawe kilima cha Yerusalema, wewe munara wa Sayuni, ambamo Mungu anafanya ulinzi juu ya watu wake, kama muchungaji juu ya kondoo wake, wewe utakuwa tena muji wenye mamlaka sawa zamani. Yerusalema utakuwa tena muji mukubwa wa mufalme. Sasa kwa nini munalia kwa sauti? Hamuna mufalme tena? Mushauri wenu ametoweka? Munalalamika kwa uchungu, kama mwanamuke anayezaa! Enyi watu wa Sayuni, mulie na kugaagaa kama mwanamuke anayezaa! Maana sasa mutaondoka katika muji huu muende kukaa katika mbuga, mutakwenda mpaka Babeli. Lakini kule, mutaokolewa. Kule Yawe atawakomboa toka katika makucha ya waadui zenu. Mataifa mengi yamekusanyika kwa kuwashambulia. Yanasema: Muache muji wao uchafuliwe, nasi tufurahie kuona uharibifu wa Sayuni! Lakini wao hawafahamu mawazo ya Yawe wala hawaelewi mupango wake: kwamba amewakusanya pamoja, kama miganda pahali pa kupepetea. Yawe anasema: Enyi watu wa Sayuni, musimame muwakanyagekanyage! Nitawapatia nguvu kama ngombe dume mwenye pembe za chuma na kwato za shaba. Mutawasaga watu wa mataifa mengi; mutanitolea mimi mapato yao, mutanitolea mali zao mimi Bwana wa dunia yote. Mujikusanye enyi watu wa Yerusalema; mukisema: Tumeshambuliwa, tumesongwa; naye mutawala wa Israeli wanamupiga fimbo kwenye shavu. Yawe anasema hivi: Lakini wewe Betelehemu katika Efurata, wewe ni mudogo tu kati ya ukoo wa Yuda, lakini kwako kutanitokea mutawala atakayetawala juu ya Israeli. Asili yake ni ya zamani sana. Hivyo Mungu atawaachilia watu wake kwa waadui, mpaka yule mwanamuke mwenye kuwa na mimba atakapozaa. Kisha wandugu zake waliobakia, watarudi na kuungana na Waisraeli wenzao. Huyo mutawala atawachunga watu wake kwa nguvu ya Yawe, kwa utukufu wa Yawe, Mungu wake. Watu wake wataishi kwa usalama, maana atakuwa mukubwa mpaka kwa miisho ya dunia. Yeye ndiye atakayeleta amani. Waasuria wakishambulia inchi yetu, na kuingia katika nyumba zetu nzuri, tutatuma walinzi wetu wapigane nao, tutawapeleka waongozi wetu kwa wingi. Kwa silaha zao wataitawala inchi ya Asuria, na kuirizi inchi ya Nimurodi. Watatuokoa toka katika mikono ya Waasuria, watakapoingia katika inchi yetu na kuanza kuishambulia. Wazao wa Yakobo watakaobaki wazima wataenea kati ya mataifa mengi, watakuwa kama umande unaotoka kwa Yawe, kama manyunyu yanayoanguka kwenye majani ambayo hayasababishwi na mutu wala kumutegemea mwanadamu. Wazao wa Yakobo watakaobaki wazima, wataenea kati ya mataifa na watu wengi watakuwa na nguvu kubwa kama simba kati ya nyama wa pori, kama simba mukali kati ya makundi ya kondoo, ambaye kila pahali anapopita, anarukia na kurarua nyama, na hakuna mutu yeyote wa kuiokoa. Waisraeli watawashinda waadui zao na kuwaangamiza kabisa. Wakati ule, nitawaondoa farasi wenu, na kuyaharibu magari yenu ya vita. –Ni ujumbe wa Yawe.– Nitaiharibu miji ya inchi yenu, na kubomoa vikingio vyenu. Nitakomesha matendo yenu ya uchawi, nanyi hamutakuwa tena na waaguzi. Nitaziharibu sanamu zenu, na nguzo zenu za ibada; nanyi mutakoma kuabudu vitu mulivyotengeneza wenyewe. Nitaziongoa sanamu za Ashera kutoka kwenu, na kuiangamiza miji yenu. Kwa hasira na kasirani yangu, nitalipiza kisasi mataifa yote yasiyonitii. Musikilize jinsi Yawe anavyosema: Wewe nabii, kwenda ukailalamikie milima, navyo vilima visikie sauti yako. Musikilize mashitaki ya Yawe, enyi milima, musikilize enyi misingi imara ya dunia! Yawe yuko na maneno juu ya watu wake. Yeye atatoa mashitaki juu ya Waisraeli. Anasema hivi: Enyi watu wangu, nimewatendea nini? Nimewachokesha kwa kitu gani? Munijibu! Mimi niliwatoa katika inchi ya Misri, niliwakomboa kutoka katika utumwa, niliwapatia Musa, Haruni na Miriamu kwa kuwaongoza. Enyi watu wangu, mukumbuke mipango mibaya ya Balaki mufalme wa Moabu, na jinsi Balama mwana wa Beori alivyomujibu. Mukumbuke yaliyotukia katika njia kati ya Sitimu na Gilgali. Mukumbuke, mutambue matendo yangu ya kuwaokoa! Nimwendee Yawe na kitu gani, nipate kumwabudu Mungu anayekuwa juu? Nimwendee na sadaka za kuteketezwa kwa moto, nimutolee mwana-ngombe wa mwaka mumoja? Yawe atapendezwa nikimutolea maelfu ya kondoo dume, au mito elfu na elfu ya mafuta? Nimutolee muzaliwa wangu wa kwanza kwa ajili ya kosa langu, mutoto wangu wa kwanza kwa ajili ya zambi yangu? Mungu amekuonyesha yanayokuwa mema, ewe mwanadamu; kitu Yawe anachotaka kwako ni hiki: kutenda mambo ya haki, kupenda kuwa na huruma, na kuishi kwa unyenyekevu mbele ya Mungu wako. Yawe anawaita wakaaji wa muji, na ni jambo la hekima sana kumutii yeye: Musikilize, enyi watu wa Yuda; musikilize enyi muliokusanyika katika muji. Nitavumilia maovu yaliyolundikwa ndani ya nyumba yao, mali zilizopatikana kwa udanganyifu, na matumizi ya vipimo vya udanganyifu, jambo ambalo ni chukizo? Ninaweza kusema kwamba hawana kosa watu wanaotumia vipimo vya udanganyifu na mawe ya kupimia yasiyokuwa ya kweli? Watajiri wa miji ni watesaji wakali kabisa, wakaaji wake wanasema uongo, kila neno wanalosema ni udanganyifu. Kwa hiyo nami, nimeanza kuwaangusha chini, na kuwaangamiza kwa sababu ya zambi zenu. Mutakula lakini hamutashiba; njaa itazidi kuwa katika tumbo yenu. Mukiweka akiba haitachungwa, na mukichunga kitu nitakiharibu kwa vita. Mutapanda mbegu, lakini hamutavuna. Mutakamua mafuta ya zeituni, lakini hamutatumia mafuta hayo. Mutakamua zabibu, lakini hamutakunywa divai hiyo. Ninyi munafuata mufano mubaya wa mufalme Omuri na mufano mubaya wa jamaa ya mwana wake, Ahabu, na mumefuata mashauri yao. Kwa hiyo nitawaletea maangamizi, na kila mutu atawazarau. Watu watawachekelea kila pahali. Ole wangu! Mimi ninakuwa kama muvunaji kisha wakati wa mavuno; hakuna tini za kwanzakwanza ninazotamani. Ni kama wakati wa kuchuma zabibu: hakuna hata fungu moja la zabibu la kula! Hakuna mutu mwaminifu kwa Mungu aliyebaki katika inchi, hakuna mutu yeyote mwenye usawa kati ya watu. Kila mumoja anavizia kumwanga damu; kila mumoja anamwinda mwenzake kusudi amunase. Wote ni wafundi wa kutenda maovu; waongozi na waamuzi wanaomba kituliro. Wakubwa wanaonyesha wazi nia zao mbaya, nao wanashirikiana pamoja kwa kuzitimiza. Mutu muzuri zaidi kati yao ni kama michongoma, naye mwenye usawa zaidi ni hatari kama upango wa miiba. Siku iliyongojewa ya azabu yao imefika. Na sasa mahangaiko yamewapata. Usimwaminie mwenzako, wala usimutumainie rafiki yako. Chunga mudomo wako, usimwambie kitu muke wako wewe mwenyewe. Maana, mutoto mwanaume anamuzarau baba yake; mutoto mwanamuke anabishana na mama yake, muke wa mwana anapingana na mama mukwe wake. Waadui wa mutu ni watu wa nyumba yake. Lakini mimi ninamutumainia Yawe, ninamutazamia Mungu mwenye kuniokoa; Mungu wangu atanisikiliza. Usifurahie hali yangu ewe adui yangu! Nikianguka, nitasimama tena; nikiwa katika giza, Yawe ni mwangaza wangu. Kwa vile nimemukosea Yawe, nitavumilia kasirani yake, mpaka atakapotetea maneno yangu na kunijalia haki yangu. Atanileta inje kwenye mwangaza, nami nitaona akisimamisha haki. Halafu adui yangu ataona hayo naye atafunikwa na haya; maana aliniambia: Basi Yawe, Mungu wako, yuko wapi? Mimi mwenyewe nitamwona adui akianguka; atakanyagwakanyagwa chini kama matope katika njia. Siku inakuja ambapo kuta za muji wenu zitajengwa upya. Siku hiyo mipaka ya inchi yenu itapanuliwa. Siku hiyo wandugu zenu watawarudilia, kutoka Asuria na vijiji vya Misri, kutoka inchi ya Misri na eneo la muto Furati; kutoka sehemu za maji na sehemu za milima. Lakini inchi yote nyingine itakuwa jangwa, kwa sababu ya uovu wa wakaaji wake. Ee Mungu, uwachunge watu wako kwa fimbo yako, uwachunge wale wanaokuwa kundi lako mwenyewe ambao wanaishi peke yao katika pori na kuzungukwa na inchi yenye mboleo. Uwachunge kama ulivyofanya pale zamani katika shamba la malisho ya Basani na Gileadi. Kama wakati ulipotutoa toka katika inchi ya Misri, utuonyeshe tena maajabu yako. Nao watu wa mataifa watakapoona hayo, watafezeheka hata kama wana nguvu. Watapigwa na bumbuazi na kukosa cha kusema na kuwa kama viziwi. Watatambaa katika mavumbi kama nyoka, kama viumbe vinavyotambaa. Watatoka katika makimbilio yao wakitetemeka na kujaa hofu. Watakugeukia Yawe, Mungu wetu, kwa hofu, wataogopa kwa sababu yako. Ee Mungu, ni nani anayekuwa kama wewe? Wewe unasemehe zambi za watu wako waliobaki, wala hauyaangalii makosa yao. Hasira yako haidumu milele, lakini unapendelea zaidi kutuonyesha wema wako. Utatuhurumia tena; utatupilia mbali zambi zetu, utazitupa zote katika vilindi vya bahari. Utatuonyesha uaminifu na wema wako sisi wazao wa Abrahamu na wa Yakobo, kama ulivyowaahidi babu zetu tangu zamani. Ujumbe wa Mungu juu ya Ninawe. Kitabu cha maono ya Nahumu wa Elkosi. Yawe ni Mungu mwenye wivu, anayelipiza kisasi; Yawe analipiza kisasi na ni mwenye kasirani; Yawe analipiza kisasi kwa wapinzani wake, kasirani yake inawaka juu ya waadui zake. Yawe hakasiriki upesi, lakini amejaa nguvu, Yawe hatawaachilia wenye makosa hata kidogo. Yawe anapopita, upepo mukali na zoruba vinatokea; mawingu ni mavumbi yanayonyanyuliwa na miguu yake. Anaikaripia bahari na kuikausha, yeye anaikausha mito yote. Mbuga za Basani na mulima Karmeli zinanyauka, maua ya Lebanoni yanakauka. Milima inatetemeka mbele yake, vilima vinayeyuka. Dunia inatetemeka mbele yake, ulimwengu na vyote vinavyokuwa ndani yake. Nani anayeweza kusimama mbele ya kasirani ya Yawe? Nani anayeweza kuvumilia ukali wa hasira yake? Yeye anaimwanga hasira yake inayowaka kama moto, hata mawe makubwa anayapasua vipandevipande. Yawe ni muzuri, yeye ni kimbilio la usalama wakati wa taabu. Yeye anawalinda wote wanaokimbilia usalama kwake. Waadui wakishambulia inchi kama mafuriko, yeye anawaangamiza; anawafuatilia na kuwafukuza mpaka katika giza. Mbona munafanya mipango juu ya Yawe? Yeye atawakomesha na kuwaangamiza, wala mupinzani wake hataweza kusimama tena. Watateketezwa kama kichaka cha miiba, wao wanaoikalia kulewa. Watateketezwa kama vile majani yenye kukauka. Ndani yako kumetoka mumoja aliyepanga maovu juu ya Yawe. Huyu mutu anafanya shauri baya sana. Yawe anasema hivi: Ingawa Waasuria ni wengi na wenye nguvu, wao wataangushwa na kuangamizwa. Ingawa nimewatesa ninyi watu wangu, sitawatesa tena zaidi. Sasa nitaivunja nira ya Asuria katika shingo lenu, na minyororo waliyowafungia nitaikatakata. Yawe ameamuru hivi juu ya Ninawe: Hautapata wazao kwa kulidumisha jina lako. Sanamu zako za kuchonga na za chuma chenye kuyeyushwa, nitazivunjavunja katika nyumba za miungu yako. Mimi nitakuchimbia kaburi lako, maana wewe haufai kwa kitu chochote. Enyi watu wa Yuda muangalie: Mutu anakuja kutoka milima anayeleta habari njema, anayetangaza amani. Mufanye sikukuu zenu, mutimize viapo vyenu, maana waovu hawatawashambulia, kwa sababu wameangamizwa kabisa. Mwangamizaji amekuja kukushambulia, ee Ninawe. Chunga kuta zako! Weka ulinzi katika barabara! Ujiweke tayari! Kusanya nguvu zako zote! Yawe anamurudishia Yakobo utukufu wake, anawapa tena Waisraeli utukufu wao, ingawa washambulizi hawakuwaachia kitu, hata matawi yao ya mizabibu waliyakata. Ngao za mashujaa wake ni nyekundu, waaskari wake wamevaa nguo nyekundu sana. Magari yao ya vita yanametameta kama ndimi za moto, yamepangwa tayari kwa kushambulia; farasi hawatulii kwa hamu ya kushambulia. Magari ya vita yanakimbia mbio katika barabara, yanakwenda huko na huko katika uwanja. Yanametameta kama ndimi za moto! Yanakwenda mbio kama umeme. Sasa anawaita wakubwa wake, nao wanajikwaa wanapomwendea; wanakwenda kwenye ukuta kwa haraka kutayarisha ukingo. Vikingio vya mito vimefunguliwa, nyumba ya kifalme imejaa hofu. Muji uko wazi kabisa, watu wamekamatwa mateka. Wanawake wake wanaomboleza, wanalia kama njiwa, na kujipigapiga kwenye vifua. Muji Ninawe ni kama birika lililobomoka, watu wake wanaukimbia ovyo. Musimame! Musimame! Sauti inaita, lakini hakuna anayerudi nyuma. Munyanganye feza, munyanganye zahabu! Mali yake haina mwisho! Kuna wingi wa kila kitu cha bei kali! Muji wa Ninawe ni maangamizi matupu na uharibifu! Watu wamekufa moyo, magoti yanagongana, nguvu zimewaishia, nyuso zimebadilika! Basi lile pango la simba limekuwa namna gani, lile lililokuwa maficho ya simba wakali? Ile nafasi ya simba imekuwa namna gani, nafasi ya wana-simba ambayo hakuna aliyeweza kuwashitua? Simba dume amewararulia watoto wake nyama ya kutosha, akiwakamatia simba dike nyama zao; ameyajaza mapango yake na nyama, na makao yake vipande vya nyama. Mimi Yawe wa majeshi nitakushambulia: nitayateketeza kwa moto magari yako ya vita, nitawamaliza kwa upanga hao simba wako wakali, vitu ulivyonyanganya nitavikomesha kutoka katika inchi, na sauti ya wajumbe wako haitasikilika tena. Ole wako muji wa mauaji! Umejaa udanganyifu mutupu na wizi tele, haukomi hata kidogo kunyanganya. Sikia! Mulio wa fimbo, mashindo ya magurudumu, vishindo vya farasi na ngurumo za magari ya vita! Waaskari wapanda-farasi wanashambulia, panga na mikuki inametameta; waliouawa hawana hesabu, kuna maiti nyingi sana; watu wanajikwaa juu ya maiti! Ninawe! Wewe umekuwa kama kahaba. Umewashawishi watu, ewe binti wa uchawi, uliyeyafanya mataifa kuwa watumwa kwa ukahaba wako, na watu wa mataifa kwa uchawi wako. Mimi Yawe wa majeshi ninasema nitakushambulia; nitapandisha nguo yako mpaka kwenye kichwa, niyaache mataifa yauone uchi wako, falme zitaona haya yako. Nitakutupia uchafu, na kukuzaraulisha, na kukufanya kuwa mushangao kwa watu. Kisha wote watakaokuona watakukimbia wakisema: Ninawe umeangamizwa, ni nani atakayekuomboleza? Nani atakayekufariji? Wewe Ninawe, ni bora kuliko Tebe, muji uliojengwa pembeni ya muto Nili? Tebe ulizungukwa na maji, bahari ilikuwa kikingio chake, maji yalikuwa ukuta wake! Inchi ya Kushi ilikuwa nguvu yake; nayo Misri vilevile, tena bila mwisho, watu wa Puti na Libya waliusaidia. Hata hivyo, ulikamatwa mateka, watu wake wakapelekwa katika uhamisho. Hata watoto wake walipondwapondwa katika maingilio ya kila barabara; watu wake wenye heshima waligawanywa kwa kuwapigia kura, wakubwa wake wote walifungwa minyororo. Ninawe, nawe vilevile utalewa; utamukimbia adui na kujaribu kujificha. Kuta zako zote ni kama tini za kwanza; zikitikiswa zinamwangukia mwenye kula katika kinywa. Angalia, waaskari wako ni wanawake tu. Milango ya inchi yako ni wazi mbele ya waadui zako; moto umeteketeza kabisa vifungio vyake. Muteke maji mukuwe tayari kwa kuzungukwa na vita; muimarishe vikingio vyenu. Muponde matope, mutayarishe furu ya kuchomea matofali! Lakini kule vilevile moto utawateketeza, upanga utawamaliza kabisa; utawamaliza kama nzige wanavyokula. Muongezeke kama nzige, mwongezeke kama mapanzi! Wachuuzi wako waliongezeka kuliko nyota; lakini sasa wametoweka kama vile mapanzi wanavyoruka. Wakubwa wako ni kama mapanzi, majemadari wako kama kundi la nzige; wakati wa baridi wanakaa kwenye kuta, lakini jua linapotokea, wanaruka, wala hakuna anayejua nafasi walipokwenda. Ewe mufalme wa Asuria, wachungaji wako wamelala, waheshimiwa wako wamesinzia. Watu wako wametawanyika kwenye milima, wala hakuna yeyote wa kuwakusanya. Hakuna wa kutunza mapigo yako, vidonda vyako ni vya kifo. Wote wanaosikia habari zako wanashangilia. Maana ni nani aliyeponyoka kila mara uovu wako? Haya ni maono ambayo nabii Habakuki aliyofunuliwa na Mungu. Ee Yawe, nitakulilia mpaka wakati gani, nawe usinisikilize na kunisaidia? Kwa nini ninalia “Mateso makali!” nawe hautuokoi? Kwa nini unaniachilia kuona mabaya na taabu? Uharibifu na mateso makali vinanizunguka, ugomvi na mabishano yanatokea. Hivyo sheria haina nguvu, wala haki haifuatiliwi. Waovu wanawazunguka wenye haki, hivyo hukumu inatolewa na sheria imepotoshwa. Mungu akasema: Muangalie mataifa, muone! Mustaajabu na kushangaa. Maana ninatenda kitu ukiwa bado unaishi, kitu ambacho ungeambiwa haungesadiki. Maana ninawachochea Wakaldea, taifa lile kali na lenye nguvu, taifa linalopita katika inchi yote, kwa kunyanganya makao ya watu wengine. Wao ni watu wa kuchukiza na kutisha; wao wanajiamulia sheria wenyewe na kujipatia mamlaka. Farasi wao ni wepesi kuliko chui, wakali kuliko imbwa wa pori wenye njaa. Waaskari wapanda-farasi wao wanatoka mbali, wanaruka mbio kama tai anavyorukia nyama. Wote wanakuja kwa kutesa kwa ukali; wanafukuzia wakikaza macho mbele, wanakusanya wafungwa wengi kama muchanga. Wanawachekelea wafalme, na kuwazarau watawala. Kila kuta kwao ni muzaha, wanailundikia udongo na kuiteka. Kisha wanasonga mbele kama upepo, wanapita na kufanya makosa. Nguvu zao ndio mungu wao! Wewe si ndiwe Yawe, tangu zamani sana? Wewe ndiwe Mungu wangu, Mutakatifu wangu, usiyekufa. Ee Yawe, umewachagua Wakaldea watuhukumu! Ewe kimbilio letu, umewaimarisha kusudi watuazibu! Wewe ni mutakatifu kabisa, hauwezi kutazama uovu, hauwezi kuvumilia hata kidogo kuona mabaya. Mbona basi unawaona wafanya maovu na kunyamaza, kwa nini unanyamaza waovu wanapowamaliza wale watu wanaokuwa wenye haki kuliko wao? Umewafanya watu kama samaki katika bahari, kama viumbe vinavyotambaa visivyokuwa na mwongozi! Wakaldea wanawavua watu kwa ndoana, wanawakokotea inje kwa nyavu zao, wanawakusanya wote katika wavu wao, kisha wanafurahi na kushangilia. Kwa hiyo, wanazitambikia nyavu zao, na kuzifukizia ubani; maana kwa njia ya vitu hivyo mapato yao yanaongezeka, na wanakuwa na chakula kingi. Hawataacha hata kidogo kuvuta upinde wao? Wataendelea tu kuwanasa watu, na kuyaangamiza mataifa bila huruma? Mimi nitasimama pahali pa kuchungulia, na kuikaa juu katika munara; nitakaa macho wazi nipate kuona ataniambia nini, atajibu nini juu ya malalamiko yangu. Kisha, Yawe akanijibu hivi: Uyaandike maono haya; uyaandike wazi juu ya vibao, anayepitia pale apate kuyasoma haraka. Maono haya yanangoja wakati uliopangwa; ni maono ya ukweli juu ya mwisho. Kama yanaonekana kuchelewa, uyangojee; hakika yatafika, wala hayatachelewa. Andika: Uwaangalie wenye kiburi, hao wataangamia; lakini wenye haki wataishi kwa kumwamini Mungu. Zaidi ya hayo, divai inapotosha; mutu mwenye kiburi hatadumu. Yuko tayari kuwameza wengine kama kuzimu; kama vile kifo, hatosheki na kitu. Anajikusanyia mataifa yote, na watu wote kama mali yake. Kila mutu atamuchekelea mutu wa namna hiyo na kumutungia misemo ya kitambi: Ole wako unayejilundikia visivyokuwa vyako, na kutwaa rehani mali za watu lakini haulipi! Utaendelea kufanya hivyo mpaka wakati gani? Siku moja wale waliokukopesha watasimama kwa rafla, wale wanaokutetemesha wataamuka. Halafu utakuwa mateka wao. Wewe umenyanganya mataifa mengi, lakini wote wanaobaki watakunyanganya wewe, kwa mauaji na mateso uliyoitendea dunia, uliyoifanyia miji na wakaaji wake wote. Ole wako unayejitajirisha kwa hasara ya mwingine, unayejenga nyumba yako juu katika milima ukizani kuwa salama mbali na hasara. Lakini kwa mipango yako umefezehesha jamaa lako. Kwa kuyaangamiza mataifa mengi, umeyaangamiza maisha yako mwenyewe. Ndiyo maana hata mawe yatalalamika juu ya ukuta, na miti ya nyumba itayaunga mukono. Ole wako unayejenga muji kwa mauaji unayesimika kijiji kwa maovu! Yawe wa majeshi anasababisha juhudi za watu zipotelee katika moto, na mataifa yajishugulishe bure. Utukufu wa Yawe utaenea pote katika dunia, kama vile maji yanavyoenea katika bahari. Ole wako unayewalewesha jirani zako, na kutia sumu katika divai yao kusudi upate kuwaona wakiikaa uchi. Utajaa haya pahali pa heshima. Utakunywa wewe mwenyewe na kupepesuka! Yawe mwenyewe atakulewesha, na haya itaifunika heshima yako! Mateso uliyoyatenda kule Lebanoni yatakulemea wewe; uliwaua nyama, nyama nao watakuogopesha. Yote hayo yatakupata wewe, kwa mauaji na mateso uliyoitendea dunia, uliyoifanyia miji na wakaaji wake wote. Sanamu mutu aliyotengeneza inafaa kwa nini? Sanamu ni madini yaliyoyeyushwa, ni kitu cha kueneza udanganyifu! Mutengenezaji wa sanamu anatumainia kile alichotengeneza mwenyewe, sanamu ambayo haiwezi hata kusema! Ole wake mutu anayeambia kipande cha muti: Amuka! au jiwe bubu: Simama! Sanamu inaweza kumufundisha mutu? Angalia imepakwa zahabu na feza, lakini haina uzima wowote. Lakini Yawe yuko katika hekalu lake takatifu; dunia yote ikae kimya mbele yake. Maombi ya nabii Habakuki: Ee Yawe, nimesikia juu ya utukufu wako, juu ya matendo yako, nami ninaogopa. Uyafanye tena mambo yale wakati wetu; uyafanye yajulikane wakati huu wetu. Unapokasirika tafazali ukumbuke huruma yako! Mungu amekuja kutoka jimbo la Temani, Mungu mutakatifu anakuja kutoka mulima Parani. Utukufu wake umeenea pote mbinguni, nayo dunia imejaa sifa zake. Anangaa kama jua; mishale ya mwangaza inatoka katika mukono wake ambamo nguvu yake inajificha. Ugonjwa mukali unatangulia mbele yake, nyuma yake hasara inafuata. Akisimama dunia inatikisika; akiyatupia mataifa jicho, hayo yanatetemeka. Milima ya milele inavunjwavunjwa, vilima vya zamani za kale vinaanguka; ni juu yao kulipokuwa njia zake za kale na kale. Niliwaona watu wa Kusani wakiteseka, na watu wa Midiani wakitetemeka. Ee Yawe, umeikasirikia mito? Umeyakasirikia maji ya bahari? Ulipanda juu ya gari lako la vita na kuendesha farasi kwa kupata ushindi. Uliuweka tayari upinde wako, ukaweka mishale yako kwenye kamba. Uliupasua udongo kwa mito. Milima ilikuona, ikanyauka; mafuriko ya maji yakapita mule. Vilindi vya bahari vilinguruma, na kurusha juu mawimbi yake. Jua na mwezi vilikaa kimya katika makao yao, vilipoona mwangaza wa mishale yako ikienda mbio, vilipouona mukuki wako ukimetameta. Kwa kasirani ulipita juu ya inchi, uliyakanyaga mataifa kwa hasira yako. Ulitoka kwenda kuwaokoa watu wako, kumwokoa yule uliyemusimika kwa kumupakaa mafuta. Ulimuponda mutawala wa jamii ya waovu, ukawaangamiza kabisa wafuasi wake. Umetoboa vichwa vya wakubwa wao kwa mikuki yao wenyewe, waliotufikia kama zoruba kututawanya, wakijivuna kwa kuwameza wamasikini kwa siri. Kwa farasi wako ulitembea juu ya bahari, bahari inayosukwasukwa na mawimbi. Nikasikia hayo, matumbotumbo yangu yakatetemeka. Midomo yangu inatetemeka kwa hofu, mifupa yangu inateguka, miguu yangu inatetemeka. Ninangojea kwa utulivu siku ile ya hasara, ambayo inawafikia wale wanaotushambulia. Hata kama miti ya tini isipochanua maua wala mizabibu kuzaa zabibu, hata kama mizeituni isipozaa zeituni na mashamba yasipotoa chakula, hata kama kondoo wakitoweka katika zizi na nyama wa kufugwa kukosekana katika mazizi, mimi nitaendelea kumufurahia Yawe. Nitamushangilia Mungu anayeniokoa. Bwana, Yawe ndiye nguvu yangu, anaimarisha miguu yangu kama ya paa, ananiwezesha kupita juu katika milima. Kwa mwimbishaji: pamoja na ala za muziki wa nyuzi. Hili ni neno la Yawe lililomufikia Zefania mwana wa Kusi, mujukuu wa Gedalia mwana wa Amaria, wa uzao wa mufalme Hezekia, wakati wa utawala wa mufalme Yosia mwana wa Amoni, mufalme wa Yuda: Nitateketeza kabisa viumbe vyote katika dunia: wanadamu, nyama, ndege na samaki. Vyote nitaviangamiza. Waovu nitawaangamiza kabisa; wanadamu nitawateketeza kabisa katika dunia. Nitaunyoosha mukono wangu kwa kuazibu inchi ya Yuda, pamoja na wakaaji wote wa Yerusalema. Nitaangamiza mabaki yote ya mungu Bali kutoka inchi hii, na hakuna atakayetambua jina lao. Nitawaangamiza wote wanaoinama juu ya dari, wakiabudu jeshi la mbinguni. Nitawaangamiza wale wanaoniabudu na kuapa kwa jina langu, tena wanaapa vilevile kwa jina la mungu Milkomu. Nitawaangamiza wote walioniacha mimi Yawe, wote walioacha kunitafuta na kuniuliza shauri. Munyamaze mbele ya Bwana wenu Yawe, maana siku ya Yawe iko karibu. Yawe ametayarisha sadaka, naye amekwisha kutakasa waalikwa wake. Yawe anasema hivi: Katika siku ile ya karamu yangu, nitawaazibu wakubwa wa watu hao, vilevile na wana wa mufalme pamoja na wote wanaoiga desturi za kigeni. Siku hiyo nitawaazibu wote wanaoruka kizingiti cha nyumba kama wapagani, wanaojaza nyumba ya bwana wao vitu vya mateso na udanganyifu. Siku hiyo, kutasikilika kilio kutoka Mulango wa Samaki, maombolezo kutoka Mutaa wa Pili, na mulio mukubwa kutoka katika milima. –Ni ujumbe wa Yawe.– Mulie, enyi wakaaji wa Makitesi! Wachuuzi wote wameangamia, wote wanaopima feza wameteketezwa. Wakati huo nitauchunguza Yerusalema kwa taa, nitawaazibu wanaoishi wakitulia kama machicha ya divai, wote ambao wanasema kati yao: Yawe hatafanya kitu: chema au kibaya. Utajiri wao utanyanganywa, na nyumba zao zitaachwa tupu! Watajijengea nyumba, lakini hawataishi humo. Watapanda mizabibu, lakini hawatakunywa divai yake. Ile siku kubwa ya Yawe imekaribia, iko karibu na inakuja mbio. Mulio wa siku ya Yawe ni wa uchungu; hapo, hata shujaa atalia kwa sauti. Siku hiyo itakuwa siku ya kasirani, ni siku ya taabu na uchungu, siku ya giza na huzuni; siku ya uharibifu na maangamizi, siku ya mawingu na giza kubwa. Siku hiyo ni ya mulio wa baragumu ya vita, juu ya miji yenye vikingio na kuta ndefu. Kwa maana watu wamemukosea Yawe, yeye atawaletea taabu kubwa, wao watatembea kama vipofu. Damu yao itamwangwa kama mavumbi, na miili yao kama mavi. Feza yao wala zahabu yao havitaweza kuwaokoa katika siku hiyo ya kasirani ya Yawe. Kwa moto wa wivu wake dunia yote itateketezwa. Kwa ukamilifu na kwa namna ya kuogopesha atawafanya wakaaji wote katika dunia watoweke. Mukusanyike, mukusanyike, enyi taifa la watu wasiokuwa na haya, mbele hamujapeperushwa mbali kama maganda, mbele haijawafikia siku ya hasira kali ya Yawe, mbele haijawafikia siku ya kasirani ya Yawe. Mutafute Yawe, enyi wanyenyekevu wote katika inchi, enyi munaozitii amri zake. Mutafute haki, mutafute unyenyekevu; labda mutaiponyoka siku ya kasirani ya Yawe. Muji wa Gaza utahamwa, muji wa Askeloni utakuwa tupu. Wakaaji wa Asidodi watafukuzwa muchana, na wale wa Ekroni wataongolewa. Ole wenu wakaaji wa inchi za pembeni ya bahari, watu wanaoishi kule Krete! Yawe amesema juu yenu, enyi wakaaji wa Kanana, inchi ya Wafilistini: Mimi nitawaangamiza wala hakutabaki hata mukaaji mumoja! Nanyi inchi ya pembeni ya bahari mutafanywa kuwa shamba la malisho; mutakuwa vibanda vya wachungaji na mazizi ya kondoo. Inchi ya pembeni ya bahari itakuwa makao ya mabaki ya ukoo wa Yuda. Watachunga nyama wao kule. Nyumba za muji wa Askeloni zitakuwa pahali pao pa kulala. Maana mimi Yawe, Mungu wao nitawakumbuka na kuwarudishia hali yao njema. Nimeyasikia matusi ya Wamoabu na mazarau ya Waamoni, jinsi walivyowatusi watu wangu na kujivuna kwamba wamenyanganya inchi yao. Kwa hiyo, kama vile ninavyoishi, –ni ujumbe wa Yawe wa majeshi, Mungu wa Israeli– inchi ya Moabu itakuwa kama Sodoma na ya Amoni itakuwa kama Gomora. Inchi zake zitakuwa shamba la miiba na mashimo ya chumvi, zitakuwa ukiwa milele. Watu wangu watakaobaki wataziteka, watu wa taifa langu waliobaki watazirizi. Hayo yatakuwa malipo ya kiburi chao, kwa sababu waliwachekelea na kujivuna mbele ya watu wa Yawe wa majeshi. Wao watamwogopa sana Yawe; ataiangamiza miungu yote ya dunia. Mataifa yote katika dunia yatamwabudu; kila taifa katika pahali pake. Nanyi watu wa Kushi vilevile mutauawa kwa upanga. Yawe atanyoosha mukono wake kwa kuazibu inchi ya upande wa kaskazini, na kuiangamiza inchi ya Asuria. Ataufanya muji wa Ninawe kuwa ukiwa, kuwa pahali penye kukauka kama jangwa. Makundi ya nyama wa kufugwa watalala ndani yake, vilevile kila nyama wa pori. Tai, nyangenyange na korongo wataishi juu ya nguzo zake, bundi watalia kwenye madirisha yake, vibombobombo watalia kwenye vizingiti, maana nyumba zake za mierezi zitakuwa tupu. Basi huu ndio muji uliojivuna na kuishi kwa usalama, muji uliojisemesha: Ni mimi tu, hakuna mwingine! Jinsi gani umekuwa mutupu na makao ya nyama wa pori! Kila mutu anayepita karibu atauzomea na kuuzarau. Ole wake Yerusalema, muji wa uasi, muchafu, na wenye kujaa watesaji. Hausikilizi onyo lolote, wala haukubali kutii. Haukumutegemea Yawe hata kidogo, wala kumukaribia Mungu wake. Wakubwa wake ni simba wanaonguruma, waamuzi wake ni imbwa wa pori wenye njaa magaribi wasioacha chochote mpaka asubui. Manabii wake ni watu wasiojali na wadanganyifu. Makuhani wake wamevichafua vitu vitakatifu na kuivunja sheria kwa nguvu. Lakini Yawe anayekuwa katika muji ule ni mwenye haki, yeye hatendi jambo lolote baya. Kila siku asubui anatangaza hukumu yake, kila kunapopambazuka anaitimiza. Lakini waovu hawana haya hata kidogo. Yawe anasema: Nimeyateketeza kabisa mataifa; kuta zao za kujikinga ni mabomoko. Barabara zao nimeziharibu, na hakuna anayepita ndani yake. Miji yao imekuwa mitupu, bila watu, na bila wakaaji. Nilisema: Hakika katika muji huu watanitii na kukubali kuonywa; hawataacha kukumbuka mara hizo zote nilizowaazibu. Lakini watu wake walizidisha tamaa zao za kufanya matendo yao kuwa upotovu. Kwa hiyo muningojee mimi Yawe, ngoja siku nitakaposimama kutoa mashitaki. Nimeamua kuyakusanya mataifa na falme, kuyamwangia kasirani yangu, na ukali wa hasira yangu. Dunia yote itateketezwa kwa moto wa kasirani yangu. Wakati huo nitabadilisha luga ya watu, nitawawezesha kusema luga safi kusudi waniite mimi Yawe, na kuniabudu kwa moyo mumoja. Kutoka ngambo ya mito ya Kushi watu wangu wanaoniomba, wale ambao wametawanyika, wataniletea sadaka yangu. Siku hiyo, hautapata haya kutokana na matendo yako ya kuniasi, maana nitawaondoa kati yako wale wanaojivuna na kujitukuza, nawe hautakuwa na kiburi tena kwenye mulima wangu mutakatifu. Nitakuachia watu wapole na wanyenyekevu ambao watakimbilia usalama kwangu mimi Yawe. Waisraeli watakaobaki hawatatenda mabaya wala hawatasema uongo, wala kwao hakutapatikana mudanganyifu yeyote. Watapata chakula na kulala wala hakuna mutu atakayewaogopesha. Imba kwa sauti, ewe Sayuni, piga vigelegele, ee Israeli. Furahi na kushangilia kwa moyo wote, ewe Yerusalema! Yawe amekuondolea hukumu iliyokuwa juu yako, amewafukuza waadui zako. Yawe, mufalme wa Israeli yuko pamoja nawe. Hautaogopa tena hasara. Siku hiyo, Yerusalema utaambiwa: Usiogope, ee Sayuni, usilegee mikono. Yawe, Mungu wako, yuko pamoja nawe. Yeye ni shujaa anayekuletea ushindi. Yeye atakufurahia kwa furaha kubwa. Kwa upendo wake atakujalia uzima mupya. Atakufurahia kwa wimbo wa sauti kubwa, kama vile katika siku ya sikukuu. Yawe anasema: Nitakuondolea hasara zako, nawe hautahitaji kupata haya kwa ajili yake. Wakati huo, nitawaazibu wote wanaokugandamiza. Nitawaokoa vilema na kuwakusanya waliotupwa na kubadilisha haya yao kuwa sifa na utukufu katika dunia yote. Wakati huo nitawakusanya, na kuwafanya mujulikane na kusifiwa kati ya watu wote katika dunia, na kuwarudishia hali yenu njema, nanyi mutaona kwa macho yenu wenyewe. –Ni Yawe anayesema hivyo. Katika mwaka wa pili wa utawala wa mufalme Dario wa Persia, siku ya kwanza ya mwezi wa sita, kwa njia ya nabii Hagai, neno la Yawe liliwafikia Zerubabeli mwana wa Saltieli pamoja na Kuhani Mukubwa Yoshua mwana wa Yosadaki kusema hivi: Yawe wa majeshi anasema hivi: Watu hawa wanasema kwamba wakati wa kuijenga upya nyumba ya Yawe haujafika. Neno la Yawe lilifika kwa njia ya nabii Hagai kusema hivi: Ni sawa kwenu kukaa katika nyumba zenu nzuri wakati nyumba yangu ni mabomoko matupu? Basi, Yawe wa majeshi anasema hivi: Mufikiri vizuri juu ya namna munavyofanya! Munapanda mbegu kwa wingi, lakini munavuna kidogo. Munakula, lakini hamushibi. Munakunywa divai, lakini hamutosheki. Munavaa nguo, lakini bado munasikia baridi. Mushahara wa mutumishi unakuwa kama umetumbukizwa katika mufuko uliotoboka. Yawe wa majeshi anasema hivi: Mufikiri vizuri juu ya namna munavyofanya! Sasa basi muende kwenye milima mulete miti, muijenge upya nyumba yangu, nipate kuifurahia na kutukuzwa. –Ni Yawe anayesema hivyo. Mulitazamia mavuno mengi, lakini mulipata kidogo tu. Mulipoyaleta kwenye nyumba, niliyapeperusha mbali. Kwa nini? Kwa sababu nyumba yangu ni mabomoko matupu wakati kila mumoja wenu anashugulikia nyumba yake. Ndiyo maana mbingu zimeacha kunyesha mvua, nao udongo hauoteshi mavuno. Nimeleta ukavu katika inchi, juu ya vilima na mashamba ya ngano, mashamba ya mizabibu na mashamba ya mizeituni na kila mumea, watu na nyama, na chochote mulichokitoshea jasho. –Ni ujumbe wa Yawe wa majeshi. Halafu Zerubabeli mwana wa Saltieli, na Kuhani Mukubwa Yoshua mwana wa Yosadaki, pamoja na watu wote waliokuwa wamerudi kutoka katika uhamisho wakafanya kama vile Yawe, Mungu wao alivyowaambia na kama vile walivyoambiwa na Hagai, yule nabii aliyetumwa na Yawe, Mungu wao. Watu wakamuheshimia Yawe. Kisha Hagai, mujumbe wa Yawe, akawapa watu ujumbe huu kutoka kwa Yawe: Mimi niko pamoja nanyi. –Ni ujumbe wa Yawe. Basi, Yawe akamutia moyo mutawala Zerubabeli wa Yuda pamoja na Kuhani Mukubwa Yoshua na watu wote waliokuwa wamerudi kutoka katika uhamisho. Wakaanza kazi hiyo ya kuijenga upya nyumba ya Yawe wa majeshi, Mungu wao, katika siku makumi mbili na ine ya mwezi wa sita, mwaka wa pili wa utawala wa mufalme Dario. Katika siku makumi mbili na moja, mwezi wa saba mwaka uleule, neno la Yawe lilifika kwa njia ya nabii Hagai na kusema hivi: Sema na mutawala wa Yuda, Zerubabeli mwana wa Saltieli, Kuhani Mukubwa Yoshua mwana wa Yosadaki na watu waliorudi kutoka katika uhamisho uwaambie hivi: Ni nani kati yenu anayekumbuka jinsi nyumba hii ilivyokuwa yenye utukufu? Sasa munaiona namna gani? Bila shaka sasa munaiona kama si kitu. Hata hivyo, ujipe moyo, ewe Zerubabeli. –Ni ujumbe wa Yawe. Ujipe moyo, Kuhani Mukubwa Yoshua mwana wa Yosadaki. Mujipe moyo nanyi watu wote wa inchi hii. –Ni ujumbe wa Yawe! Mufanye kazi, maana mimi niko pamoja nanyi. –Ni ujumbe wa Yawe wa majeshi! Mulipotoka Misri niliwaahidi kwamba nitakuwa pamoja nanyi siku zote. Basi, ningali pamoja nanyi, kwa hiyo, musiogope kitu. Yawe wa majeshi anasema hivi: Kisha muda kidogo nitazitikisa mbingu na dunia, bahari na inchi kavu. Nitayatikisa mataifa yote na mali zao zote zitaletwa humu, nami nitaifanya nyumba hii kuwa yenye utukufu. –Ni Yawe wa majeshi anayesema hivyo. Feza na zahabu yote katika dunia ni mali yangu. –Ni ujumbe wa Yawe. Nyumba mupya itakuwa yenye utukufu zaidi kuliko ile ya kwanza. –Ni Yawe wa majeshi anayesema hivyo! Kutoka hapa nitawapa watu wangu fanaka. –Ni ujumbe wa Yawe wa majeshi! Katika siku ya makumi mbili na ine ya mwezi wa kenda, katika mwaka wa pili wa utawala wa Dario, neno la Yawe wa majeshi lilimufikia nabii Hagai kusema hivi: Yawe wa majeshi anasema hivi: Makuhani watoe uamuzi juu ya jambo hili: Kama mutu akibeba kipande cha nyama iliyotakaswa katika upindo wa nguo yake, kisha akigusa kwa upindo wa nguo ile mukate au chakula kilichopikwa, au divai, au mafuta au chakula cha aina yoyote ile, basi, chakula hicho kitakuwa kitakatifu? Makuhani wakamujibu: Hapana. Hagai akawauliza tena: Mutu anayehesabiwa kuwa muchafu kwa kugusa maiti, akigusa sehemu ya vyakula hivi, chakula hicho kitakuwa kichafu? Makuhani wakamujibu: Ndiyo, kitakuwa kichafu. Hagai akajibu na kusema hivi: Hivi ndivyo inavyokuwa kwa watu wa taifa hili mbele yangu –ni ujumbe wa Yawe– na kila kitu wanachofanya; hata vitu wanavyotoa kwenye mazabahu ni vichafu. Lakini sasa mufikiri vizuri juu ya mambo yatakayotukia. Mbele ya kuanza kujenga upya nyumba yangu, hali yenu ilikuwa namna gani? Mutu alifika kwenye fungu la ngano akingojea kupata vipimo makumi mbili, lakini kulikuwa vipimo kumi tu. Mutu alifika kwenye mutungi wa divai akingojea kujaza vyombo makumi tano, lakini kulikuwa makumi mbili tu. Mimea yenu yote muliyojaribu kupanda, niliiharibu kwa kuikausha na kwa kuipiga kwa ukungu na mvua ya mawe, lakini hata hivyo hamukunirudilia. –Ni ujumbe wa Yawe.– Sasa, mufikiri vizuri juu ya mambo yatakayotukia. Leo ni siku makumi mbili na ine ya mwezi wa kenda, siku ambayo musingi wa hekalu umekamilika. Basi mufikiri vizuri: Ingawa sasa hakuna ngano ndani ya gala, nayo mizabibu, tini, mikomamanga na mizeituni haijazaa kitu, lakini tangu leo, nitawabariki. Siku ileile ya makumi mbili na ine, mwezi wa kenda, neno la Yawe lilimufikia Hagai kwa mara ya pili kusema hivi: Sema na Zerubabeli mutawala wa Yuda umwambie hivi: Nitazitikisa mbingu na dunia na kuangusha falme na kukomesha nguvu zao. Nitayapindua magari yao ya vita na waaskari wapanda-farasi wake, nao wataanguka na kuuana wao kwa wao. Siku hiyo, nitakutwaa wewe Zerubabeli mwana wa Saltieli, mutumishi wangu. –Ni ujumbe wa Yawe wa majeshi! Nitakusimika utawale kwa jina langu. –Ni ujumbe wa Yawe! Wewe ndiwe niliyekuchagua. –Ni ujumbe wa Yawe wa majeshi! Katika mwezi wa nane wa mwaka wa pili wa utawala wa mufalme Dario wa Persia, neno la Yawe lilimufikia nabii Zakaria mwana wa Berekia, mujukuu wa Ido kusema hivi: Yawe alichukizwa sana na babu zenu. Basi, uwaambie watu kwamba: Yawe wa majeshi anasema hivi: Munirudilie nami nitawarudilia ninyi. –Ni Yawe wa majeshi anayesema. Musikuwe kama babu zenu. Manabii waliwaambia: Yawe anasema hivi: muachane na mienendo yenu miovu na matendo yenu mabaya. Lakini wao hawakunisikiliza wala hawakunitii. –Ni ujumbe wa Yawe.– Babu zenu, wako wapi? Na manabii, wanaishi milele? Babu zenu hawakupata azabu kwa sababu ya kukataa maagizo yangu na amri nilizowapa kwa njia ya watumishi wangu manabii? Wakati huo, wao waligeuka na kusema kwamba: Yawe wa majeshi alikusudia kututendea kulingana na mienendo yetu na matendo yetu, na kweli ndivyo alivyotutendea. Katika siku makumi mbili na ine ya mwezi wa kumi na moja, ni kusema mwezi wa Sebati, mwaka wa pili wa utawala wa Dario, neno la Yawe lilimufikia nabii Zakaria mwana wa Berekia, mujukuu wa Ido. Zakaria akasema hivi: Wakati wa usiku, nilimwona malaika akipanda juu ya farasi mwekundu. Malaika yule alikuwa akisimama katika bonde, katikati ya miti ya mihadasi. Nyuma yake kulikuwa farasi wengine wekundu, wa kijivujivu na weupe. Basi, nikamwuliza: Bwana, farasi hawa wana maana gani? Malaika yule aliyesema nami akaniambia: Nitakuonyesha wale farasi wana maana gani. Hawa ndio waliotumwa na Yawe kuichunguza dunia. Hao farasi wakamwambia huyo malaika wa Yawe aliyekuwa akisimama katikati ya miti ya mihadasi: Tumeichunguza dunia yote, nayo kweli imetulia. Halafu yule malaika wa Yawe akasema: Ee Yawe wa majeshi, kwa muda gani utaendelea kutokuwa na huruma juu ya muji Yerusalema na miji ya inchi ya Yuda ambayo umeikasirikia kwa muda wa miaka makumi saba? Yawe akamupa yule malaika jibu jema na lenye matumaini. Basi, huyo malaika akaniambia: Tangaza kwa sauti na kusema hivi: Yawe wa majeshi anasema hivi: Ninasikia wivu sana juu ya Yerusalema na Sayuni. Lakini nimekasirikia sana mataifa ambayo yanastarehe. Nilikuwa ninayakasirikia kidogo, lakini yaliwaongezea hasara. Kwa hiyo, Yawe anasema hivi: Ninarudilia Yerusalema kwa huruma; humo itajengwa nyumba yangu, na ujenzi mupya wa muji utaanza. –Ni Yawe ya majeshi anayesema. Kisha malaika yule akaniambia nitangaze ujumbe huu mwingine: Yawe wa majeshi anasema hivi: Miji yake itafurika tena na fanaka. Yawe atafariji tena Sayuni, atachagua Yerusalema kuwa wake. Katika maono mengine, niliona pembe ine. Nami nikamwuliza yule malaika aliyezungumuza nami: Pembe hizi zina maana gani? Yeye akanijibu: Pembe hizi zina maana ya yale mataifa ambayo yaliwatawanya watu wa Yuda, Israeli na Yerusalema. Kisha, Yawe akanionyesha wafuachuma wane. Nami nikauliza: Watu hawa wanakuja kufanya nini? Yeye akanijibu: Watu hawa wamekuja kuyatisha na kuyaangamiza yale mataifa yenye nguvu ambayo yaliishambulia inchi ya Yuda na kuwatawanya watu wake. Katika maono mengine, nilimwona mutu aliyekuwa na kamba ya kupima katika mukono wake. Basi, nikamwuliza: Unakwenda wapi? Naye akanijibu: Ninakwenda kuupima urefu na upana wa Yerusalema. Yule malaika aliyezungumuza nami akaenda kukutana na malaika mwingine ambaye alikuwa anakuja kwake. Basi, huyo malaika aliyezungumuza nami akamwambia yule mwenzake: Kimbia umwambie yule kijana kwamba si lazima Yerusalema ukuwe na kuta, kama sivyo hapatakuwa nafasi ya kuwatoshelea wakaaji wake wengi na nyama watakaokuwa ndani yake. Yawe anasema kwamba yeye mwenyewe atakuwa ukuta wa moto kwa kuulinda muji huo pande zote, naye atakaa mule kwa utukufu wake. Yawe anasema hivi: Mukimbie kutoka katika inchi ya kaskazini ambako mimi nilikuwa nimewatawanya kila upande. Haraka! Ninyi wote munaokaa katika inchi ya Babeli, mukimbilie Sayuni! Yawe wa majeshi, ambaye kwa utukufu wake amenituma, anasema hivi juu ya mataifa yaliyowakamata mateka watu wake: Hakika, anayewagusa ninyi anagusa mboni ya jicho langu. Kweli, nitawashambulia wale waliowakamata mateka, nao watakamatwa mateka na wale waliowafanya watumwa wao. Halafu kwa hiyo mutajua kwamba Yawe wa majeshi ndiye aliyenituma. Yawe anasema hivi: Enyi watu wa Sayuni, muimbe na kufurahi kwa maana ninakuja na kukaa kati yenu. Mataifa mengi yatajiunga nami Yawe, nao watakuwa watu wangu; nami nitakaa kati yenu. Halafu mutajua kwamba Yawe wa majeshi ndiye aliyenituma kwenu. Watu wa Yuda watakuwa tena mali ya pekee ya Yawe katika inchi takatifu, na Yerusalema itakuwa tena muji wake aliouchagua. Enyi wanadamu wote, munyamaze mbele ya Yawe, maana, yeye anakuja kutoka makao yake matakatifu. Katika maono mengine, Yawe alinionyesha Kuhani Mukubwa Yoshua akisimama mbele ya malaika wa Yawe, na kwa upande wake wa kuume Shetani alisimama kwa kumushitaki. Malaika wa Yawe akamwambia yule Shetani: Yawe akulaani, ewe Shetani! Kweli, Yawe aliyechagua Yerusalema akulaani! Huyu ni kama kipande cha kuni kilichoopolewa ndani ya moto! Kuhani Mukubwa Yoshua alikuwa akisimama mbele ya malaika, akiwa amevaa nguo zenye kuchafuka. Malaika akawaambia watumishi wake: Muvue Kuhani Mukubwa Yoshua nguo zake zenye kuchafuka. Kisha akamwambia Kuhani Mukubwa Yoshua: Nimeiondoa zambi yako, nami nitakupatia nguo za bei kali. Kisha akawaambia wamuvalishe kitambaa safi juu ya kichwa. Hivyo, wakamuvalisha kitambaa safi na nguo; naye malaika wa Yawe alikuwa akisimama pale. Malaika wa Yawe akamwonya Kuhani Mukubwa Yoshua, akamwambia: Yawe wa majeshi anasema hivi: Ukifuata njia zangu na kushika maagizo niliyokupa, basi, utaisimamia nyumba yangu na viwanja vyake. Nami nitakuwezesha kuingia katika utumishi wangu kama hawa wanaosimama mbele yangu. Sasa sikiliza kwa uangalifu, ewe Yoshua, Kuhani Mukubwa; musikilize vilevile enyi makuhani wenzake munaokuwa pamoja naye, ninyi munaokuwa kitambulisho cha wakati muzuri unaokuja: Nitamuleta mutumishi wangu anayeitwa Tawi. Mukumbuke kwamba nimeweka mbele ya Yoshua jiwe moja lenye nyuso saba. Nami nitachora maandiko juu yake, na kwa siku moja tu, nitaiondoa zambi ya inchi hii. Kweli, ni mimi Yawe wa majeshi ninayesema hivyo. Siku hiyo, kila mumoja wenu atamwalika mwenzake kufurahia amani na utulivu katika shamba lake la mizabibu na la tini. Yule malaika aliyeongea nami, akanifikia tena, akaniamusha kama vile kumwamusha mutu toka katika usingizi. Akaniuliza: Unaona nini? Nami nikamujibu: Ninaona kinara cha taa cha zahabu. Juu yake kuna bakuli la mafuta na taa saba, na kila moja ina pahali pa kutilia tambi saba. Karibu na kinara hicho kuna miti miwili ya muzeituni; mumoja upande wa kuume na mwingine upande wa kushoto. Basi, nikamwuliza yule malaika: Bwana, vitu hivi vina maana gani? Naye akanijibu: Haujui maana ya vitu hivi? Nikamujibu: Sijui bwana wangu. Yule malaika akaniambia vilevile niseme neno hili la Yawe juu ya Zerubabeli: Hauwezi kushinda kwa nguvu au kwa uwezo wako mwenyewe, lakini kwa musaada wa roho wangu. –Ni Yawe wa majeshi anayesema. Tena, akaongeza kusema: Mulima huu ni kizuizi? Hapana! Wewe Zerubabeli utausawazisha. Wewe utaanzisha ujenzi mupya wa hekalu, na wakati utakapoliweka jiwe la mwisho, watu watashangilia wakisema: Ni zuri! Kweli, ni zuri! Neno la Yawe lilinifikia kusema hivi: Zerubabeli ameuweka musingi wa hekalu naye vilevile atalikamilisha. Hayo yatakapotukia, watu wangu watajua kwamba mimi Yawe wa majeshi ndimi niliyekutuma kwao. Maendeleo ya ujenzi wa hekalu yanaonekana madogo, na watu wanayazarau; lakini watamwona Zerubabeli akiendelea kulijenga hekalu, nao watafurahi. Sasa, juu ya hizo taa saba, yule malaika akaniambia: Ni macho saba ya Yawe yanayoona kila nafasi katika dunia. Nami nikazidi kuuliza: Hiyo miti miwili ya mizeituni inayokuwa upande wa kuume na wa kushoto wa kinara, ina maana gani? Na yale matawi mawili pembeni ya mirija miwili ya zahabu ambamo mafuta ya mizeituni yanatiririkia, yana maana gani? Naye akaniambia: Haujui? Nami nikamujibu: Hapana, sijui Bwana! Halafu akaniambia: Hawa ndio wale watu wawili ambao Bwana wa ulimwengu wote aliwachagua kwa kuwapakaa mafuta kusudi wamutumikie. Nilipoangalia tena niliona kitabu kinaruka katika anga. Yule malaika akaniuliza: Unaona nini? Nami nikamujibu: Ninaona kitabu kinaruka katika anga; urefu wake ni metre kenda na upana wake ni metre ine na nusu. Basi, yeye akaniambia: Ndani ya kitabu hicho kumeandikwa laana ambayo inchi nzima itakayoipata. Upande mumoja imeandikwa kwamba wizi wote watafukuzwa katika inchi, na upande mwingine imeandikwa kwamba wote wenye kuapa uongo watafanyiwa vile vile. Yawe wa majeshi anasema kwamba yeye mwenyewe ataipeleka laana hiyo. Itapenya kila nyumba ya mwizi na kila nyumba ya mwenye kuapa uongo kwa kutumia jina lake; itakaa mule na kuteketeza nyumba hiyo yote, mbao na mawe. Yule malaika aliyeongea nami alinikaribia, akaniambia: Inua macho uone kile kinachokuja. Nami nikamwuliza: Ni kitu gani hicho? Naye akanijibu: Hicho ni kikapu chenye makosa ya inchi nzima. Kikapu chenyewe kilikuwa na mufuniko uliotengenezwa kwa chuma cha risasi; kilifunuliwa, nami nikaona mwanamuke ameikaa mule ndani. Yule malaika akaniambia: Mwanamuke yule ni mufano wa uovu! Kisha yule malaika akamusukumia ndani ya kikapu mwanamuke yule na kukifunika. Nilipoangalia, niliona wanawake wawili wanatokea; walikuwa wakirushwa na upepo, nao walikuwa na mabawa yenye nguvu kama ya korongo. Wanawake wale wakakiinua kile kikapu katika anga. Basi, nikamwuliza yule malaika aliyezungumuza nami: Wanakipeleka wapi kile kikapu? Naye akaniambia: Wanakipeleka katika inchi ya Sinari. Kule watakijengea hekalu na litakapokuwa tayari, watakiweka kikapu hicho ndani. Niliona maono mengine tena. Niliona magari mane ya vita yakitoka katikati ya milima miwili ya shaba nyeusi. Gari la kwanza lilikokotwa na farasi wekundu, la pili lilikokotwa na farasi weusi, la tatu lilikokotwa na farasi weupe, na la ine lilikokotwa na farasi wa kijivujivu. Basi, nikamwuliza yule malaika aliyeongea nami: Bwana, magari haya ya vita yana maana gani? Malaika akanijibu: Magari haya ni upepo kutoka pande ine za mbingu. Yalikuwa mbele ya Yawe wa dunia nzima, na sasa yanaondoka. Lile gari linalokokotwa na farasi weusi linakwenda upande wa kaskazini, lile linalokokotwa na farasi weupe linakwenda upande wa magaribi, na lile linalokokotwa na farasi wa kijivujivu linakwenda upande wa kusini. Farasi hao walipotokea walikuwa na hamu sana ya kwenda kuichunguza dunia. Naye malaika akawaambia: Basi! Muende muichunguze dunia. Basi, wakaenda na kuichunguza dunia. Kisha yule malaika aliyeongea nami akaniambia kwa sauti: Wale farasi waliokwenda katika inchi ya kaskazini wameituliza kasirani ya Yawe. Neno la Yawe lilinifikia kusema hivi: Pokea zawadi za watu wanaokuwa katika uhamisho zilizoletwa na Heldai, Tobia na Yedaya. Kwenda leo hii katika nyumba ya Yosia mwana wa Zefania ambamo watu hao wamekwenda mbele ya kufika kutoka Babeli. Utatwaa feza na zahabu hiyo, utengeneze taji ambalo utamuvalisha Kuhani Mukubwa Yoshua mwana wa Yosadaki, na kumwambia kwamba Yawe wa majeshi anasema hivi: Hapa kuna mutu anayeitwa Tawi. Yeye atastawi pale anapokuwa na kulijenga hekalu la Yawe. Yeye ndiye atakayelijenga hekalu la Yawe. Atapewa heshima ya kifalme na kuikaa kwenye kiti chake cha kifalme kuwatawala watu wake. Kuhani Mukubwa ataikaa karibu na kiti cha kifalme cha mutawala yule, nao wawili watafanya kazi pamoja kwa amani. Taji hiyo italindwa katika hekalu la Yawe kwa heshima ya Heldai, Tobia, Yedaya na Yosia mwana wa Zefania. Watu wanaokaa katika inchi za mbali watakuja kusaidia kwa kulijenga hekalu langu mimi Yawe. Nanyi mutajua kwamba Yawe wa majeshi, ndiye aliyenituma kwenu. Haya yote yatatukia kama mukiitii sauti ya Yawe, Mungu wenu. Katika mwaka wa ine wa utawala wa mufalme Dario, siku ya ine ya mwezi wa kenda, ni kusema mwezi wa Kisileu, neno la Yawe lilimufikia Zakaria. Watu wa muji wa Beteli walikuwa wamewatuma Sareseri na Regemu-Meleki pamoja na watu wao kumwomba Yawe rehema zake, na kuwauliza makuhani wa hekalu la Yawe wa majeshi maneno haya: Tuendelee kuomboleza na kufunga kula chakula katika mwezi wa tano kama tulivyofanya kwa muda wa miaka mingi sasa? Halafu, neno la Yawe wa majeshi lilinifikia kusema hivi: Uwaambie wakaaji wote wa inchi na makuhani hivi: Kwa muda wa miaka makumi saba iliyopita, ninyi mulikuwa mukifunga na kuomboleza katika mwezi wa tano na wa saba. Munazani mulifunga kwa ajili yangu? Munapokula na kunywa, si munakula na kunywa kwa ajili yenu wenyewe? Haya ndiyo mambo ambayo mimi Yawe niliyowaambia kupitia kwa manabii wa zamani, wakati Yerusalema ulikuwa umestawi na wenye wakaaji tele, na wakati ambapo kulikuwa wakaaji wengi katika miji ya kandokando yake na katika eneo la Negebu na mabonde ya Sefela. Neno la Yawe lilimufikia Zakaria kusema hivi: Yawe wa majeshi anasema hivi: Mutoe hukumu kwa haki, mutende mema na kuwa na huruma ninyi kwa ninyi. Musiwatese wajane, wayatima, wageni au wamasikini; musipange kutendeana mabaya ndani ya mioyo yenu. Lakini watu walikataa kunisikiliza, waligeuza mabega na kuziba masikio yao kusudi wasisikie. Wakaifanya mioyo yao kuwa migumu kama jiwe, wasipate kusikia sheria yangu mimi Yawe wa majeshi niliyoitangaza kwa roho yangu kwa kupitia manabii waliotangulia. Kwa hiyo, mimi Yawe wa majeshi nikawaka hasira juu yao, nikasema: Kwa sababu niliwaita nao hawakunisikiliza, basi, nao waliponiita, sikuwasikiliza. Nami niliwatawanya kwa upepo mukali kati ya mataifa yote ambayo hawakuyajua. Hivyo inchi waliyoiacha ikabaki tupu; hapakuwa mutu yeyote aliyekaa mule; inchi hiyo ya kupendeza ikakuwa ukiwa. Neno la Yawe lilinifikia kusema hivi: Yawe wa majeshi anasema hivi: Ninachomwa na upendo mukubwa kwa ajili ya Sayuni, na ninawaka kasirani nyingi juu ya waadui zake. Yawe wa majeshi anasema hivi: Nitaurudilia Sayuni na kufanya makao yangu katika Yerusalema. Muji Yerusalema utaitwa “Muji Mwaminifu”, na mulima wa Yawe wa majeshi utaitwa “Mulima Mutakatifu”. Yawe wa majeshi anasema hivi: Wazee, wanaume na wanawake, wataonekana tena wakiikaa kwenye barabara za Yerusalema, kila mumoja na fimbo yake kwa sababu ya kuishi miaka mingi. Barabara za Yerusalema zitajaa vijana wanaume na wanawake, wakichezacheza mule. Yawe wa majeshi anasema hivi: Kwa watu hawa waliobaki, hali hii inaonekana kuwa kitu kisichowezekana; lakini munazani haiwezekani kwangu mimi? –Ni ujumbe wa Yawe wa majeshi. Yawe anasema hivi: Nitawaokoa watu wangu kutoka inchi ya mashariki na kutoka inchi ya magaribi na kuwafanya wakae katika Yerusalema. Wao watakuwa watu wangu, nami nitakuwa Mungu wao; nitatawala juu yao kwa uaminifu na haki. Yawe wa majeshi anasema hivi: Mujipe moyo! Sasa munayasikia maneno ambayo mulitangaziwa na manabii wakati musingi wa hekalu langu ulipowekwa kulijenga upya. Mbele ya wakati huo, watu hawakupata mushahara kwa kazi zao wala mali kwa ajili ya kutumikisha nyama. Hamukuwa na usalama kwa sababu ya waadui zenu, maana nilisababisha uadui kati ya watu wote. Lakini sasa sitawatendea hao watu wa taifa hili wanaobaki kama vile zamani. –Ni ujumbe wa Yawe wa majeshi.– Sasa nitaleta tena amani katika dunia, mvua itanyesha kama kawaida, udongo utatoa mazao, na mizabibu itazaa kwa wingi. Nitawapa watu wanaobaki wa taifa hili yale yote yakuwe mali yao. Enyi watu wa Yuda na watu wa Israeli! Wakati uliopita ninyi mulionekana kuwa watu waliolaaniwa kati ya watu wa mataifa. Lakini sasa mimi nitawaokoa, nanyi mutakuwa watu waliobarikiwa. Basi, musiogope tena, lakini mujipe moyo! Yawe wa majeshi anasema hivi: Kama nilivyokusudia kuwatendea ninyi maovu kwa sababu babu zenu walinikasirikisha wala sikuwaonea huruma, vile vile nimekusudia kuutendea wema Yerusalema na watu wa Yuda. Basi, musiogope. Hivi ndivyo munavyopaswa kufanya: Kila mumoja wenu amwambie mwenzake ukweli. Tribinali zenu zitoe siku zote hukumu za haki zinazoleta amani. Mutu yeyote asikusudie kumutendea mwenzake ubaya wala musiape uongo, maana ninayachukia sana matendo hayo. Ni mimi Yawe ninayesema hivyo. Yawe wa majeshi akanitolea mimi Zakaria ujumbe huu: Yawe wa majeshi anasema hivi: Siku za mafungo ya kula chakula ya mwezi wa ine, mwezi wa tano, mwezi wa saba na mwezi wa kumi, zitakuwa nyakati za furaha na shangwe; zitakuwa sikukuu za shangwe kwa watu wa Yuda. Basi, mupende ukweli na amani. Yawe wa majeshi anasema hivi: Watu wengi wa mataifa ya kigeni na wakaaji wa miji mingi watajaa katika Yerusalema. Wakaaji wa muji mumoja watawaendea wakaaji wa muji mwingine na kuwaambia: Tuende pamoja kumwabudu Yawe wa majeshi na kumwomba baraka! Kweli, mataifa yenye nguvu na watu wengi watakuja Yerusalema kumwabudu Yawe wa majeshi na kumwomba baraka. Yawe wa majeshi anasema hivi: Wakati ule, watu kumi kutoka mataifa ya kila luga watamukamatilia Muyuda mumoja na kushika nguo yake na kumwambia: Tunataka kwenda pamoja nanyi, kwa sababu tumesikia kwamba Mungu yuko pamoja nanyi. Ujumbe wa Yawe: Neno la Yawe ni juu ya azabu ya miji Hadiraki na Damasiki. Maana inchi ya Aramu ni mali ya Yawe, kama vile makabila yote ya Israeli yanavyokuwa, vilevile muji wa Hamati unaopakana na Hadiraki, na hata miji ya Tiro na Sidona ingawa inajiona kuwa na hekima sana. Muji wa Tiro umejijengea kuta kubwa, umejilundikia feza kama mavumbi, na zahabu kama takataka katika barabara. Lakini Bwana atatwaa mali yake yote, atautumbukiza utajiri wake katika bahari, na kuuteketeza muji ule kwa moto. Muji wa Askeloni utaona hayo na kuogopa, nao muji wa Gaza utagaagaa kwa uchungu; hata Ekroni, maana tumaini lake litatoweka. Gaza utapoteza mufalme wake, nao Askeloni hautakaliwa na watu. Muji wa Asidodi utakaliwa na wana haramu. Yawe anasema hivi: Nitakikomesha kiburi cha Wafilistini. Nitawakomesha kula nyama yenye damu, na chakula ambacho ni chukizo. Watakaobaki watakuwa mali yangu, kama ukoo mumoja katika Yuda. Watu wa Ekroni watakuwa kama Wayebusi. Mimi mwenyewe nitailinda inchi yangu, nitazuia majeshi yasipitepite ndani. Hakuna mutu atakayewatesa tena watu wangu, maana, kwa macho yangu mwenyewe, nimeona jinsi walivyoteseka. Mushangilie sana enyi watu wa Sayuni! Mupige vigelegele, enyi watu wa Yerusalema! Angalia, mufalme wenu anawakujia, anakuja kwa shangwe na ushindi! Ni mupole, amepanda juu ya punda, juu ya mwana-punda, mutoto wa punda. Ataondoa kabisa magari ya vita katika inchi ya Efuraimu, na farasi wa vita kutoka katika Yerusalema; pinde za vita zitatupwa mbali. Naye ataleta amani kati ya mataifa; utawala wake utaenea toka bahari mpaka bahari, toka muto Furati hata miisho ya dunia. Yawe anasema hivi: Kwa sababu ya agano langu pamoja nanyi, agano lililokamilishwa kwa njia ya damu, nitawakomboa wafungwa wenu wanaokuwa kama wamefungwa katika shimo tupu. Enyi wafungwa wenye tumaini, murudi kwenye ukuta wa muji wenu. Sasa mimi ninawatangazia: nitawarudishia mema mara mbili. Yuda nitamutumia kama upinde wangu; Efuraimu nimemufanya mushale wangu. Ee Sayuni, watu wako nitawatumia kama upanga kwa kuwashambulia watu wa Ugriki; watakuwa kama upanga wa shujaa. Yawe atawatokea watu wake; atafyatua mishale yake kama umeme. Bwana wetu Yawe atapiga baragumu; atafika pamoja na upepo mukali wa kusini. Yawe wa majeshi atawalinda watu wake, nao watawaangamiza waadui zao. Watapiga kelele katika vita kama walevi, wataimwanga damu ya waadui zao. Itatiririka kama damu ya nyama wanaotolewa kwa sadaka iliyomiminwa juu ya mazabahu kutoka ndani ya bakuli. Wakati ule, Yawe, Mungu wao, atawaokoa, maana wao ni kundi lake; nao watangaa katika inchi yake kama mawe ya bei kali katika taji. Angalia jinsi gani uzuri na urembo wake unavyokuwa! Vijana wanaume na wanawake watastawi kwa wingi wa ngano na divai mupya. Muombe Yawe awape mvua za masika. Yawe ndiye anayeleta mawingu ya mvua; ndiye anayewapa watu mvua za manyunyu, na kustawisha mimea katika shamba kwa ajili ya wote. Sanamu zao za kupigia ramuli ni uongo mutupu, na waaguzi wao wanaagua uongo; watabiri wao wanatabiri ndoto danganyifu, na kuwapa watu faraja za bure. Ndiyo maana watu wa Yuda wanatangatanga kama kondoo; wanataabika maana wamekosa muchungaji. Yawe anasema hivi: Nimewaka hasira juu ya hao wachungaji, nami nitawaazibu hao watawala. Mimi Yawe wa majeshi, nitalitunza kundi langu, ukoo wa Yuda. Nitawafanya kuwa farasi wangu hodari wa vita. Kwa ukoo wa Yuda kutatokea: watawala wa kila namna, wakubwa wenye nguvu kama jiwe kubwa la musingi, wanaokuwa imara kama musumari wa hema, wenye nguvu kama upinde wa vita. Watu wa Yuda watakuwa kama mashujaa katika vita, watawakanyaga waadui zao ndani ya matope katika njia. Watapigana kwa sababu mimi Yawe nipo pamoja nao; nao watawafezehesha hata waaskari wapanda-farasi. Nitawaimarisha watu wa Yuda; nitawaokoa wazao wa Yosefu. Nitawarudisha kwao kwa maana ninawaonea huruma, nao watakuwa kama vile sikuwa nimewakataa. Mimi ni Yawe, Mungu wao, nami nitayasikiliza maombi yao. Watu wa Efuraimu watakuwa kama mashujaa katika vita; watajaa furaha kama watu waliokunywa divai. Watoto wao wataona hayo na kufurahi, watajaa furaha ndani ya moyo kwa sababu yangu mimi Yawe. Nitawaita watu wangu na kuwakusanya pamoja; nimekusudia kuwakomboa, nao watakuwa wengi kama vile mbele. Japo niliwatawanya kati ya mataifa, hata hivyo, watanikumbuka wakiwa humo. Nao pamoja na watoto wao wataishi na kurudi katika nyumba zao. Nitawarudisha kutoka inchi ya Misri, nitawakusanya kutoka Asuria; nitawaleta katika inchi ya Gileadi na Lebanoni, nao watajaa kila nafasi katika inchi. Watapitia katika bahari ya mateso, nami nitayapiga mawimbi yake, na vilindi vya maji ya muto Nili vitakauka. Kiburi cha Asuria kitavunjwa na nguvu za Misri zitatoweka. Mimi nitawaimarisha watu wangu, nao watanitii na kuishi kwa kunipendeza. Ni mimi Yawe ninayesema hivyo. Fungua milango yako, ewe Lebanoni kusudi moto uiteketeze mierezi yako! Muomboleze, enyi misunobari, kwa sababu mierezi imeteketea. Miti hiyo mitukufu imeharibiwa! Enyi mialo ya Basani, muomboleze, kwa maana pori kubwa limekatwa! Sikia maombolezo ya watawala! Utukufu wao umeharibiwa! Sikia ngurumo za simba! Pori la muto Yordani limeharibiwa! Yawe, Mungu wangu, alisema hivi: Ujifanye muchungaji wa kondoo wanaokwenda kuchinjwa. Wanunuzi wao wanawachinja lakini hawaazibiwi; na wanaowauzisha wanasema: “Yawe ashukuriwe! Sasa tumetajirika.” Hata wachungaji wenyewe hawawaonei huruma. Sitawahurumia tena wakaaji wa dunia. Nitamwacha kila mutu katika mikono ya mwenzake, na kila mwanainchi katika mikono ya mufalme wake. Nao wataiangamiza dunia, nami sitamwokoa mutu yeyote toka katika mikono yao. –Ni ujumbe wa Yawe. Basi, nikakuwa muchungaji wa kondoo ambao wachuuzi waliwatayarisha kwenda kuchinjwa. Nikatwaa fimbo mbili: moja nikaiita “Rehema”, na ingine nikaiita “Umoja”, nikaenda kuchunga kondoo. Kwa muda wa mwezi mumoja, nikaua wachungaji watatu wabaya. Tena uvumilivu wangu kwa kondoo ukaniishia, nao kwa upande wao, wakanichukia. Basi, nikawaambia: “Sitakuwa muchungaji wenu tena. Atakayekufa akufe! Atakayeangamia aangamie! Na wale watakaobaki wakulane wao kwa wao.” Nikakamata ile fimbo yangu niliyoiita “Rehema”, nikaivunja, kuonyesha kwamba agano Yawe alilofanya na watu wake limevunjwa. Na agano hilo likavunjwa siku ileile. Wale wachuuzi wa kondoo waliokuwa wananiangalia, wakajua kwamba neno la Yawe lilikuwa limenifikia. Kisha nikawaambia: Kama mukipendezwa, munilipe mushahara wangu; lakini kama munaona sivyo, basi muache. Basi, wakanipimia vikoroti makumi tatu vya feza kwa mushahara wangu. Kisha Yawe akaniambia: Mushahara huo ni malipo kwa kazi yangu? Basi, uzitie katika hazina ya hekalu. Hivyo nikatwaa hivyo vikoroti makumi tatu vya feza, nikavitia katika hazina ya hekalu la Yawe. Kisha nikavunja ile fimbo yangu ya pili niliyoiita “Umoja” na hivyo nikauvunja umoja kati ya Yuda na Israeli. Yawe akaniambia tena: Ujifanye tena kuwa muchungaji, lakini mara hii ukuwe kama muchungaji mupumbafu! Maana nitaleta katika inchi muchungaji asiyemujali kondoo anayeangamia, au kumutafuta kondoo anayetangatanga, au kumutunza aliyeumizwa wala kumukulisha yule anayekuwa muzima: lakini atakula wale kondoo wanono, hata kwato zao. Ole wake muchungaji mupumbafu, ambaye anawaachilia kondoo wake! Upanga uukate mukono wake, na jicho lake la kuume liongolewe! Mukono wake upooze, jicho lake la kuume lipofuke. Ujumbe wa Yawe unaoelekea Israeli. Yawe aliyezitandaza mbingu, aliyeiweka misingi ya dunia na kumupa mwanadamu uzima anasema hivi: Nitaufanya Yerusalema kuwa kama kikombe cha divai; na mataifa yanayokuwa kandokando yake yatakunywa na kuyumbayumba kama walevi. Muji Yerusalema utakaposhambuliwa, hata miji yote ya Yuda itashambuliwa. Siku hiyo nitaufanya Yerusalema kuwa kama jiwe zito kwa watu wote: yeyote atakayelinyanyua atajiumiza mwenyewe. Watu wa mataifa yote katika dunia wataushambulia muji ule. Siku hiyo, ninasema mimi Yawe, nitamutia hofu kila farasi, na askari mupanda-farasi wake nitamufanya kuwa mwenda-wazimu. Farasi wa mataifa mengine nitawapofusha. Lakini kabila la Yuda nitalilinda. Kwa hiyo wakubwa wa Yuda wataambiana: “Wakaaji wa Yerusalema wamepata nguvu yao kutoka kwa Yawe wa majeshi, Mungu wao.” Siku hiyo, nitawafanya wakubwa wa Yuda kuwa kama chungu chenye moto mukali katika pori, kama mwenge wa moto unaowaka kati ya miganda. Watayateketeza mataifa yote yanayokuwa kandokando yao. Lakini watu wa Yerusalema wataendelea kuishi salama katika muji wao. Nami Yawe nitasaidia kwanza jamaa za Yuda kusudi wazao wa Daudi na wakaaji wa Yerusalema wasijione kuwa wenye utukufu zaidi kuliko watu wengine wa kabila la Yuda. Siku hiyo, mimi Yawe nitawalinda wakaaji wa Yerusalema. Wanaokuwa wazaifu zaidi kati yao watakuwa na nguvu kama mufalme Daudi. Wazao wa Daudi watashika usukani kwa kuwaongoza watu wa Yuda kama Mungu, au kama malaika wa Yawe. Siku hiyo, nitayaangamiza mataifa yote yanayotaka kuushambulia Yerusalema. Halafu nitawajaza wazao wa Daudi na wakaaji wa muji Yerusalema roho ya huruma na maombi, nao watamwangalia yule waliyemutoboa kwa mukuki; watamulilia kama vile mutu anavyolia kwa kifo cha mutoto wake wa pekee, au kama vile mutu anavyomulilia kwa uchungu muzaliwa wake wa kwanza. Siku hiyo kutakuwa maombolezo makubwa katika Yerusalema kama vile maombolezo ya kumwomboleza Hadadi-Rimoni katika bonde la Megido. Inchi itaomboleza, kila ukoo utaomboleza peke yake: wanaume peke yao na wanawake peke yao, ukoo wa Daudi peke yake, ukoo wa Natani peke yake, ukoo wa Lawi peke yake na ukoo wa Simei peke yake. Jamaa zote zilizobaki zitaomboleza: wanaume peke yao na wanawake peke yao. Siku hiyo, kutatokea chemichemi ya kutakasa zambi na uchafu wa wazao wa Daudi na wakaaji wote wa Yerusalema. Wakati ule, nitaondoa majina ya sanamu za miungu katika inchi, wala hayatakumbukwa tena. –Ni ujumbe wa Yawe wa majeshi.– Na wanaojidai kuwa manabii nitawaondoa kabisa pamoja na tamaa zao za kuabudu sanamu. Mutu yeyote akijidai kuwa nabii, baba na mama yake waliomuzaa watamwambia: “Unapaswa kufa maana unasema uongo kwa jina la Yawe.” Na wale wazazi wake watamuchoma kisu akiwa anatabiri. Siku hiyo, kila nabii atapata haya kwa ajili ya maono yake anapotabiri. Hawatavaa nguo za manyoya kwa kudanganya watu, lakini kila mumoja atasema: “Mimi si nabii. Mimi ni mulimaji tu; nimerizi mashamba tangu ujana wangu.” Na mutu akimwuliza mumoja wao: “Vidonda hivi unavyokuwa navyo kwenye mikono yako vimetoka wapi?” Yeye atajibu: “Vidonda hivi nilivipata katika nyumba ya warafiki zangu.” Yawe wa majeshi anasema hivi: Amuka, ee upanga! Simama umushambulie muchungaji wangu, muchungaji anayenitumikia. Umuue muchungaji na kondoo watawanyike. Nitaunyoosha mukono wangu kwa kuwashambulia watu wazaifu. Sehemu mbili za tatu za watu katika inchi zitaangamizwa; ni sehemu moja ya tatu tu itakayobaki. Sehemu hiyo moja ya tatu itakayobaki, nitaipima na kuitakasa, kama vile mutu anavyosafisha feza, kama vile wanavyopima zahabu. Halafu wao wataniomba mimi, nami nitawajibu. Nitasema: Hawa ni watu wangu, nao watasema: Yawe, ndiye Mungu wetu. Angalia, siku ya kasirani ya Yawe inakuja. Siku hiyo, enyi watu wa Yerusalema, mali yenu itagawanywa mbele ya macho yenu. Yawe atayakusanya mataifa yote kwa kuushambulia Yerusalema. Muji utakamatwa, nyumba zenu zitatekwa, na wanawake wenu watakamatwa kwa kinguvu. Nusu ya wakaaji wa muji watapelekwa katika uhamisho, lakini nusu itakayobaki haitaondoshwa inje ya muji. Kisha Yawe atatoka na kuyapiga vita mataifa hayo, kama vile anavyofanya siku zote wakati wa vita. Siku hiyo, atasimama kwenye mulima wa Mizeituni unaokuwa upande wa mashariki wa Yerusalema. Mulima ule utagawanywa kwa sehemu mbili na bonde pana litatokea toka upande wa mashariki mpaka wa magaribi. Nusu moja itaelekea upande wa kaskazini na nusu ingine kusini. Ninyi mutakimbia kupitia bonde lile, katikati ya milima miwili ya Yawe. Mutakimbia kama vile babu zenu walivyokimbia tetemeko la inchi wakati wa utawala wa mufalme Uzia wa Yuda. Kisha Yawe, Mungu wangu, atakuja na watakatifu wote pamoja naye. Wakati ule hakutakuwa baridi wala baridi kali. Muchana utaendelea bila giza kuingia. Wakati huo unajulikana kwa Yawe peke yake. Hakutakuwa muchana wala usiku, kwa maana hata saa za magaribi mwangaza utaendelea kuwa. Wakati ule, maji ya uzima yatabubujika kutoka Yerusalema, na nusu ya maji yale yatatiririkia kwenye bahari ya mashariki, na nusu ingine kwenye bahari ya magaribi. Maji yale yataendelea kububujika wakati wa kipwa kama yanavyokuwa wakati wa mvua. Wakati huo, Yawe atakuwa ndiye mufalme pekee wa dunia yote; naye atakuwa ndiye Yawe pekee, mumoja tu, na jina lake litakuwa ndilo jina pekee. Inchi yote, tangu Geba mpaka Rimoni, upande wa kusini wa Yerusalema, itageuzwa kuwa mbuga yenye kunyooka kabisa. Lakini Yerusalema utabaki juu pahali pake tokea mulango wa Benjamina mpaka kwenye mulango wa zamani, hata kwenye mulango wa Konani, tangu munara wa Hanameli mpaka kwenye kikamulio cha mufalme. Muji Yerusalema utakaliwa na watu maana ndani yake hakutakuwa laana tena; watu watakaa kule kwa usalama. Lakini juu ya wale watu ambao walikuja kupigana na Yerusalema, hizi ndizo hasara ambazo Yawe atawaletea: Miili yao itaoza wangali wazima; macho yao yataoza yakiwa kwenye matundu yake na ndimi zao zitaoza zikiwa katika vinywa vyao. Siku ile, hofu kutoka kwa Yawe itawapata watu, na kila mutu atamushambulia mwenzake. Watu wa Yuda watapigana kwa kuulinda Yerusalema; utajiri wa mataifa yote yanayoizunguka inchi ya Yuda utakusanywa: watakusanya zahabu, feza na nguo kwa wingi sana. Hasara kubwa zitapata farasi, nyumbu, ngamia, punda na nyama wote watakaokuwa katika kambi zile za waadui. Kisha, kila mutu aliyebaki kati ya mataifa yote yaliyokuja kuushambulia Yerusalema, atakuwa akikuja Yerusalema mwaka kwa mwaka, kwa kumwabudu Yawe wa majeshi anayekuwa mufalme, na kushiriki kwa sikukuu ya Vibanda. Ikiwa kuna taifa lolote katika dunia ambalo halitakwenda Yerusalema kumwabudu Yawe wa majeshi anayekuwa mufalme, basi, mvua haitanyesha katika inchi yao. Ikiwa Wamisri watakataa kushiriki kwa sikukuu ya Vibanda, basi, Yawe atawapiga kwa ugonjwa uleule atakaowapiga nao mataifa yote yanayokataa kushiriki kwa sikukuu hiyo. Hiyo itakuwa ndiyo azabu itakayolipata taifa la Misri pamoja na mataifa yote yasiyoshiriki kwa sikukuu ya Vibanda. Wakati ule, kwenye kengele za farasi kutaandikwa maandiko haya: “Vimetolewa kwa Yawe.” Vyungu vinavyokuwa katika hekalu la Yawe vitakuwa kama mabakuli yanayokuwa mbele ya mazabahu. Kila chungu katika Yerusalema na inchi ya Yuda kitatolewa kwa Yawe wa majeshi, kusudi wote wanaotoa sadaka waweze kuvitumia kwa kupikia nyama ya sadaka. Wakati ule, hakutakuwa muchuuzi yeyote katika hekalu la Yawe wa majeshi. Ujumbe wa neno la Yawe lililowafikia Waisraeli kwa njia ya Malaki. Yawe anasema hivi: Nimewapenda ninyi siku zote. Lakini ninyi wazao wa Yakobo munaniuliza: Umetupenda namna gani? Yawe anasema hivi: Si Esau alikuwa ndugu wa Yakobo? Hata hivyo nilimupenda Yakobo na kumuchukia Esau. Nimeiharibu inchi ya milima ya Esau ambayo ni urizi wake, nikawaachia imbwa wa pori wa jangwa. Waedomu, wale wazao wa Esau, wanasema kwamba ingawa miji yao imeharibiwa, watajenga upya mabomoko yake. Lakini, Yawe wa majeshi anasema hivi: Wanaweza kuijenga upya, lakini mimi nitaibomoa tena. Watu watawaita: Taifa ovu ambalo Yawe amelikasirikia milele. Nanyi mutakapoyaona mambo yale kwa macho yenu, mutatambua na kusema: Ukubwa wa Yawe unafika hata inje ya mipaka ya inchi ya Israeli. Yawe wa majeshi anasema hivi: Mutoto anamuheshimu muzazi wake, na mutumishi anamuheshimu bwana wake. Ikiwa mimi ndiye Baba wenu, mbona munanivunjia heshima? Ikiwa mimi ni bwana wenu, mbona hamuniheshimu? Ninasema hivyo kwa ninyi makuhani munaozarau jina langu. Nanyi munauliza: Sisi tumezarau jina lako namna gani? Munalizarau kwa kunitolea kwenye mazabahu yangu sadaka ya chakula kichafu. Lakini ninyi munauliza: Tumekichafua namna gani? Munakichafua kwa kuizarau mazabahu yangu. Munaponitolea sadaka ya nyama anayekuwa kipofu, au kilema, au mugonjwa, huo si uovu? Mutawala atapendezwa au kukutendea mema ukimupa zawadi ya nyama kama yule? –Ni Yawe wa majeshi anayesema hivyo. Kwa hiyo sasa enyi makuhani, mumwombe Mungu kusudi atuhurumie. Yawe wa majeshi anasema hivi: Ikiwa munamutolea matoleo ya aina hiyo, kweli atawakubali? Heri kungepatikana mutu mumoja kati yenu ambaye angefunga milango ya hekalu kusudi musiwashe moto usiokubaliwa kwenye mazabahu yangu! Sipendezwi nanyi na sitaikubali sadaka yoyote munayonitolea. Watu wa mataifa katika dunia yote tokea upande jua linapopanda mpaka upande jua linaposhuka wanalitukuza jina langu. Kila pahali wananifukizia ubani na kunitolea sadaka zinazokubaliwa; maana jina langu linatukuzwa kati yao. Lakini ninyi munalizarau jina langu pale munapoichafua mazabahu yangu, na chakula munachotoa juu yake munakizarau. Munasema: Mambo haya yametuchokesha sana na munanizarau. Munaniletea sadaka za nyama muliopata kwa njia ya kunyanganya, au wanaokua vilema au wagonjwa. Basi, nipokee sadaka hizo toka katika mikono yenu? Alaaniwe mutu yeyote anayenidanganya, ambaye anaahidi kwa kiapo kunitolea sadaka ya nyama safi kutoka kundi lake, lakini ananitolea sadaka ya nyama mwenye kilema. Mimi ni mufalme mukubwa, na watu wa mataifa yote wananiogopa. –Ni Yawe wa majeshi anayesema hivyo. Yawe wa majeshi anawaambia makuhani: Sasa enyi makuhani, ninawaamuru hivi: Ni lazima muniheshimu mimi kwa matendo yenu. Musiponisikiliza nitawaletea laana. Vitu vyote munavyopewa kwa mahitaji yenu nitavilaani. Na kweli nimekwisha kuvilaani, kwa sababu hamushuguliki hata kidogo na maagizo yangu. Nitawaazibu watoto wenu na ninyi wenyewe kutokana na uovu wenu, na kuzipakaa nyuso zenu mavi ya nyama wenu wa sadaka. Nitawafukuza mbali nami. Hivyo mutajua kwamba nimewapa amri hii kusudi agano langu na ukoo wa Lawi likuwe la kudumu. Katika agano hilo, niliwaahidi uzima na amani na kwamba wao wanapaswa kunitii mimi, nao kwa upande wao walinitii mimi na kuogopa jina langu. Mafundisho yao yalikuwa ya kweli nao hawakufundisha uongo hata kidogo. Mimi na wao tulikaa kwa amani. Si kwamba walitenda haki tu, lakini waliwafundisha wengine kutotenda maovu. Ni kazi ya makuhani kuwafundisha watu maarifa ya kweli juu ya Mungu kusudi watu wawaendee kwa kujifunza mapenzi yangu kwao, maana makuhani ni wajumbe wa Yawe wa majeshi. Lakini ninyi makuhani mumegeuka na kuacha njia ya haki. Mafundisho yenu yamewaongoza watu wengi katika kutenda mabaya. Mumelivunja agano nililofanya nanyi. Nami vilevile nitawafanya muzarauliwe na kuchekelewa na Waisraeli, kwa sababu hamukuzifuata njia zangu, na munapowafundisha watu wangu munapendelea wamoja kati yao. –Ni Yawe wa majeshi anayesema hivyo. Sisi wote si watoto wa baba mumoja? Sisi wote hatukuumbwa na Mungu yuleyule? Mbona basi, hatuaminiani sisi kwa sisi, na tunalizarau agano Yawe alilofanya na babu zetu? Watu wa Yuda wamekosa uaminifu kwa Mungu na kutenda machukizo katika Israeli na katika Yerusalema. Wamechafua hekalu la Yawe analolipenda. Tena wameoa wanawake wanaoabudu miungu ya kigeni. Yawe awatenge mbali watu wanaofanya mambo hayo kutoka kati ya wazao wa Yakobo. Na wasishiriki hata kidogo katika kutoa ushuhuda na kuleta sadaka mbele ya Yawe wa majeshi. Zaidi ya hayo yote, munaifunika mazabahu ya Yawe kwa machozi yenu, mukilia na kuomboleza kwa sababu yeye hazikubali tena sadaka munazomutolea. Munauliza: Mbona sasa hazikubali? Yawe hazikubali kwa sababu anajua wazi kwamba umeivunja ahadi yako kwa muke wa ujana wako. Umekosa uaminifu kwake ingawa uliahidi mbele ya Mungu kwamba ungekuwa mwaminifu kwake. Mungu hakuwafanya ninyi wote wawili mukuwe mwili mumoja na roho moja? Alikusudia nini alipofanya hayo? Tuzae watoto wanaomupendeza Mungu. Kwa hiyo, muchunge uzima wenu na kuhakikisha kwamba hakuna hata mumoja wenu anayekosa uaminifu kwa muke wake. Yawe, Mungu wa Israeli, anasema hivi: Ninachukia kuachana. Ninachukia wakati mumoja wenu anapomutendea muke wake ubaya ule. Muhakikishe kwamba hakuna hata mumoja wenu anayekosa uaminifu kwa muke wake. Mumemuchokesha Yawe kwa maneno yenu matupu. Hata hivyo, munasema: Tumemuchokesha namna gani? Mumemuchokesha munaposema: Yawe anawaona kuwa wazuri watu wanaotenda mabaya; tena anawapenda. Au munapouliza: Yuko wapi yule Mungu mwenye haki? Yawe wa majeshi anasema: Ninamutuma mujumbe wangu anitangulie kunitengenezea njia. Bwana munayemutafuta atalifikia hekalu lake kwa rafla. Mujumbe munayemutazamia kwa hamu kubwa atakuja na kutangaza agano langu. Lakini ni nani atakayevumilia siku ile atakapokuja? Ni nani atakayesimama kuvumilia atakapotokea? Yeye ni kama moto mukali unaosafisha chuma; ni kama sabuni ya mwenye kufua nguo. Yeye atakuja kuhukumu kama mutu anayesafisha na kutakasa feza. Atawasafisha wazao wa Lawi, kama mutu anavyofua zahabu au feza, mpaka wamutolee Yawe sadaka zinazokubalika. Hivyo, sadaka za watu wa Yuda na wa Yerusalema zitamupendeza Yawe kama za watu wa zamani; kama katika miaka iliyopita. Yawe wa majeshi anasema: Kisha nitawakaribia kwa kuwahukumu. Sitasita kutoa ushuhuda juu ya wachawi, wazinzi, watoa ushuhuda wa uongo, wanaopunja mushahara wa watumishi, wanaowatesa wajane na wayatima, wanaozuia mugeni asipate haki yake na wale wasioniogopa mimi. Yawe wa majeshi alisema hivi: Mimi Yawe sibadiliki. Ni kwa sababu hii, ee ninyi wazao wa Yakobo, hamujateketezwa. Tangu wakati wa babu zenu, mumeyazarau masharti yangu wala hamukuyafuata. Munirudilie, nami nitawageukia. Lakini ninyi munaniuliza: Tutakurudilia namna gani? Ninawajibia hivi: Ni sawa kwa mutu kumudanganya Mungu? Hapana! Lakini ninyi munanidanganya! Ingawa hivyo ninyi munauliza: Tunakudanganya kwa namna gani? Kweli! Munanidanganya juu ya zaka na sadaka zenu. Ninyi na taifa lenu lote mumelaaniwa kwa sababu ya kunidanganya. Mulete katika gala yangu zaka yote, kusudi katika nyumba yangu kuwe chakula cha kutosha. Kisha munaweza kunijaribu. Munipime namna hiyo nanyi mutaona kama sitayafungua madirisha ya mbinguni na kuwatiririshia baraka tele. Wadudu waharibifu nitawazuia wasiyaharibu tena mazao yenu. Mizabibu yenu katika mashamba haitaacha kuzaa matunda. Halafu mataifa yote yatawaita ninyi watu waliobarikiwa, maana inchi yenu itakuwa inchi ya furaha. –Ni Yawe, Mungu Mukubwa anayesema hivyo. Yawe anasema hivi: Maneno yenu yamekuwa muzigo kwangu. Hata hivyo munasema: Tumesema nini juu yako? Ninyi mumesema: Kumutumikia Mungu hakuna faida. Kuna faida gani kuyatii maagizo ya Yawe wa majeshi, au kujaribu kumwonyesha kwamba tumekosa mbele yake kwa kutembea kama watu wanaoomboleza? Tunayoona sisi, ni kwamba wenye kiburi ndio wenye furaha siku zote. Watu waovu, ingawa wanastawi, hata wanapomujaribu Mungu, hawapati azabu. Halafu watu wanaomutii Yawe walizungumuza wao kwa wao, naye Yawe akasikia mazungumuzo yao. Mbele yake kukawekwa kitabu ambamo uliandikwa ukumbusho wa wale wanaomutii na kumuheshimu. Kisha Yawe wa majeshi akasema hivi: Hao watakuwa watu wangu. Watakuwa urizi wangu wa kipekee siku ile nitakaposimama kufanya jambo ninalokusudia. Sitawazuru kama vile baba asivyomuzuru mwana wake anayemutumikia. Pale ndipo mutakapotambua tena tofauti inayokuwa kati ya wenye haki na waovu, kati ya mutu anayemutumikia Mungu na asiyemutumikia. Yawe wa majeshi anasema hivi: Siku inakuja, nayo inawaka kama furu. Wenye kiburi na waovu wote watatupwa mule na kuteketezwa kama majani yenye kukauka; watateketea kabisa wala hakutabaki hata kitambulisho. Lakini kwa ajili yenu ninyi munaonitii, uwezo wangu wa kuokoa utawatokea kama jua linalokuwa na nguvu za uponyaji kwenye mishale yake. Mutatoka mukirukaruka kama wana-ngombe wanapotoka katika zizi lao. Siku hiyo mutawakanyagakanyaga waovu, nao watakuwa kama majivu chini ya miguu yenu. –Ni Yawe wa majeshi anayesema hivyo. Mukumbuke sheria, masharti na maagizo yangu niliyomwamuru mutumishi wangu Musa kwenye mulima Horebu, kusudi awaamuru watu wote wa Israeli. Mbele ya kufika kwa siku ile kubwa na ya kutisha, nitamutuma nabii Elia. Nabii Elia atawapatanisha wazazi na watoto wao; kama sivyo, nitakuja na kuiangamiza inchi yenu. Hivi hesabu ya vizazi vyote tangia Abrahamu mpaka Daudi ni vizazi kumi na vine, na tangia Daudi mpaka Waisraeli walipohamishwa kwenda Babeli ni vizazi kumi na vine, na tangia Waisraeli walipohamishwa kwenda Babeli mpaka kuzaliwa kwa Kristo ni vizazi kumi na vine. Hii ndiyo habari ya kuzaliwa kwa Yesu Kristo. Maria, mama yake, alikuwa muchumba wa Yosefu. Lakini mbele hawajakaa pamoja, akapata mimba kwa uwezo wa Roho Mutakatifu. Yosefu, muchumba wake, alikuwa mutu wa haki, naye hakutaka kumupatisha haya mbele ya watu, akakusudia kuachana naye kwa siri. Naye alipokuwa angali akifikiri juu ya maneno hayo, malaika wa Bwana akamutokea katika ndoto na kumwambia hivi: “Wewe Yosefu, mwana wa Daudi, usiogope kumwoa muchumba wako Maria, kwa maana mimba yake imetokana na uwezo wa Roho Mutakatifu. Yeye atazaa mutoto mwanaume, nawe utamwita jina lake Yesu, kwa maana ndiye atakayewaokoa watu wake toka katika zambi zao.” Mambo hayo yote yalitukia kusudi yatimie maneno Bwana aliyosema kwa njia ya nabii: “Angalia bikira atapata mimba, atazaa mutoto mwanaume, naye ataitwa Emanueli,” (maana yake “Mungu yuko pamoja nasi”). Na wakati Yosefu alipoamuka, akafanya sawa vile malaika wa Bwana alivyomwagiza. Akamwoa Maria. Lakini hakulala naye mpaka alipozaa yule mutoto mwanaume. Yosefu akamwita jina lake Yesu. Yesu alizaliwa Betelehemu katika Yudea wakati wa utawala wa mufalme Herode. Kisha kuzaliwa kwake, watu wenye elimu kutoka mashariki wakafika Yerusalema. Nao wakauliza: “Yuko wapi yule mutoto aliyezaliwa kuwa mufalme wa Wayuda? Tumeona nyota yake inayomutambulisha, nasi tumekuja kumwabudu.” Mufalme Herode aliposikia maneno haya, akafazaika sana pamoja na wakaaji wote wa Yerusalema. Akawakusanya wakubwa wote wa makuhani na walimu wa Sheria kwa kuwauliza wapi Kristo atakapozaliwa. Nao wakamujibu: “Betelehemu katika Yudea, kwa maana ilisemwa hivi kwa njia ya nabii: ‘Ewe Betelehemu, katika inchi ya Yuda, wewe si mudogo kabisa kati ya miji mikubwa ya Yuda, maana ndani yako atatoka mutawala, atakayechunga watu wangu, ndio Waisraeli.’ ” Basi Herode akawaita kwa siri wale wenye elimu kusudi wamujulishe hakika wakati gani nyota ile ilipotokea. Kisha akawatuma Betelehemu, akiwaambia: “Mwende mupeleleze habari kamili za mutoto yule. Nanyi mutakapomwona munijulishe kusudi mimi vilevile niende kumwabudu.” Kisha kumusikiliza mufalme, wakaondoka. Ile nyota waliyoiona tokea mashariki iliwatangulia, nayo ikaenda na kusimama juu ya pahali mutoto alipokuwa. Na wakati walipoiona wakafurahi sana. Wakaingia ndani ya nyumba, wakamwona mutoto pamoja na mama yake, Maria. Wakapiga magoti na kumwabudu mutoto. Kisha wakafungua mizigo yao na kumutolea zawadi ya zahabu, ubani na marasi. Nyuma ya maneno haya, Mungu akawaonya katika ndoto kwamba wasirudie tena kwa Herode, kisha wakarudia katika inchi yao wakipitia njia nyingine. Wale watu wenye elimu walipokwisha kwenda, malaika wa Bwana akamutokea Yosefu katika ndoto na kumwambia: “Amuka, utwae mutoto pamoja na mama yake na mukimbilie Misri. Mukae kule mpaka nitakapokuambia kwamba urudie, kwa maana Herode anamutafuta mutoto kusudi amwue.” Basi Yosefu akaamuka, akamutwaa mutoto pamoja na mama yake, nao wakaondoka usiku ule kwenda Misri. Akakaa kule mpaka Herode alipokwisha kufa, kusudi yatimie maneno haya Bwana aliyosema kwa njia ya nabii: “Nilimwita mwana wangu arudie toka Misri.” Herode alipoona kwamba wale watu wenye elimu wamemudanganya, akakasirika sana. Akatuma watu Betelehemu na popote kandokando yake kwa kuua watoto wote waliokuwa na umri wa miaka miwili na chini yake. Alifanya vile kufuatana na jinsi alivyohakikishwa na wale wenye elimu juu ya wakati nyota ilipotokea. Halafu yakatimia maneno haya yaliyosemwa kwa njia ya nabii Yeremia: “Sauti inasikilika toka Rama, kilio na malalamiko mengi. Ni Rakeli anayewalilia watoto wake, naye hataki kufarijiwa, kwa maana hawako tena.” Herode alipokuwa amekwisha kufa, malaika wa Bwana akamutokea Yosefu katika ndoto kule Misri. Akamwambia: “Amuka, utwae mutoto pamoja na mama yake, na urudie nao katika inchi ya Israeli, kwa maana wale waliotafuta kumwua wamekwisha kufa.” Basi Yosefu akaamuka, akamutwaa mutoto pamoja na mama yake na kurudia katika inchi ya Israeli. Lakini aliposikia kwamba Arkelao alitawala katika jimbo la Yudea kwa pahali pa baba yake Herode, Yosefu akaogopa kwenda kule. Na alipokwisha kuonywa katika ndoto, akaenda katika jimbo la Galilaya. Kule akakaa katika muji ulioitwa Nazareti, kusudi yatimie maneno yaliyosemwa kwa njia ya manabii: “Ataitwa mutu wa Nazareti.” Katika siku zile Yoane Mubatizaji alitokea akihubiri katika jangwa la Yudea akisema: “Mugeuke toka zambi zenu, kwa maana Ufalme wa mbinguni umekaribia!” Yoane ndiye yule Mungu aliyemutaja kwa njia ya nabii Isaya akisema: “Sauti inatangaza katika jangwa: ‘Mutengeneze njia ya Bwana, munyooshe pahali atakapopita!’ ” Yoane alikuwa akivaa nguo iliyotengenezwa na manyoya ya ngamia na mukaba wa ngozi katika kiuno. Naye alikuwa akikula nzige na asali ya pori. Watu wa Yerusalema na wa jimbo lote la Yudea, nao waliokaa fasi zote pembeni ya muto Yordani walimufikia. Waliungama zambi zao, naye Yoane aliwabatiza katika muto Yordani. Yoane alipoona Wafarisayo wengi na Wasadukayo wakimufikia kwa kubatizwa, aliwaambia: “Ninyi kikundi cha nyoka! Ni nani aliyewaambia kwamba munaweza kuponyoka azabu ya Mungu inayokaribia? Basi muonyeshe kwa njia ya matendo kwamba mumegeuka toka zambi zenu. Musijifikiri kwamba munaweza kujidai tu kuwa Abrahamu ndiye babu yenu. Ninawaambia kwamba Mungu anaweza kugeuza mawe haya kuwa watoto wa Abrahamu! Shoka limekwisha kuwekwa tayari kwenye mashina ya miti. Kila muti usiozaa matunda mazuri utakatwa na kutupwa katika moto. Mimi ninawabatiza kwa maji kwa kuonyesha kwamba mumegeuka toka zambi zenu. Lakini yule atakayekuja nyuma yangu atawabatiza kwa Roho Mutakatifu na kwa moto. Yeye ni mwenye uwezo kunipita, nami sistahili hata kumuvua viatu. Yeye anashika lungo katika mikono yake kwa kupepeta ngano. Atakusanya ngano na kuitia katika gala yake, lakini atateketeza maganda katika moto usiozimika.” Wakati ule Yesu akatoka Galilaya na kufika kwenye muto Yordani, akamwendea Yoane kusudi abatizwe naye. Lakini Yoane akamukatalia, akimwambia: “Ni mimi ninayepaswa kubatizwa nawe; namna gani unakuja kwangu?” Lakini Yesu akamujibu: “Ukubali kufanya hivi sasa. Kwa maana ni kwa njia hii tutatimiza mambo yote yanayokuwa ya haki mbele ya Mungu.” Basi Yoane akakubali. Yesu alipokwisha kubatizwa na kutoka ndani ya maji, mara moja mbingu zikafunguka, naye akamwona Roho wa Mungu akishuka kwa mufano wa njiwa na kukaa juu yake. Na sauti ikasikilika toka mbinguni, ikisema: “Huyu ni Mwana wangu mupendwa; ninapendezwa naye sana.” Kisha Roho Mutakatifu akamwongoza Yesu kwenda katika jangwa kusudi ajaribiwe na Shetani. Naye Yesu alipomaliza kufunga kula chakula kwa muda wa siku makumi ine, muchana na usiku, akasikia njaa. Shetani akamufikia na kumwambia: “Kama wewe ni Mwana wa Mungu, amuru mawe haya yageuke kuwa mikate.” Yesu akamujibu: “Imeandikwa hivi katika Maandiko Matakatifu: ‘Mutu hawezi kuishi kwa mukate tu, lakini kwa njia ya kushika kila neno Mungu analosema.’ ” Halafu Shetani akamupeleka katika Yerusalema, muji mutakatifu, akamusimamisha kwenye pembe la juu sana la hekalu, na kumwambia: “Kama wewe ni Mwana wa Mungu, ujitupe chini; kwa maana imeandikwa: ‘Mungu atawaamuru wamalaika wake na watakubeba katika mikono yao, kusudi muguu wako usijikwae juu ya jiwe.’ ” Yesu akamujibu: “Imeandikwa hivi vilevile: ‘Usimujaribu Bwana Mungu wako.’ ” Shetani akamupeleka tena mpaka juu ya mulima murefu, akamwonyesha falme zote za dunia na utajiri wao. Halafu akamwambia: “Nitakupa hivi vyote, kama ukipiga magoti mbele yangu na kuniabudu.” Lakini Yesu akamwambia: “Toka wewe, Shetani! Kwa maana imeandikwa: ‘Umwabudu Bwana Mungu wako na umutumikie yeye peke yake.’ ” Basi Shetani akamwacha Yesu, nao wamalaika wakakuja kushugulika naye. Yesu aliposikia kwamba Yoane ametiwa katika kifungo, akaenda zake Galilaya. Yeye akatoka Nazareti, akaenda kukaa Kapernaumu, pembeni ya ziwa la Galilaya, katika wilaya ya Zebuluni na ya Nafutali, kusudi yatimie maneno yaliyosemwa kwa njia ya nabii Isaya: “Inchi ya Zebuluni na ya Nafutali, kufuata barabara inayokwenda kwenye ziwa, ngambo ya magaribi ya Yordani, katika jimbo la Galilaya, inchi ya watu wa mataifa mengine. Watu hao wanaokaa katika giza, mwangaza umewatokea! Hao wanaoishi katika inchi yenye giza nzito sana ya lufu, wameona mwangaza mukubwa.” Tangia wakati huo Yesu akaanza kuhubiri, akisema: “Mugeuke toka zambi zenu, kwa maana Ufalme wa mbinguni umekaribia!” Yesu alipokuwa akitembea pembeni ya ziwa la Galilaya, akawaona wavuvi wawili, waliokuwa wandugu wa tumbo, Simoni (aliyeitwa Petro) na ndugu yake Andrea. Walikuwa wakitupa nyavu katika ziwa. Yesu akawaambia: “Munifuate, nami nitawaweka kwa kazi ya kuopoa watu.” Mara moja wakaacha nyavu zao, na kumufuata. Yesu alipoendelea mbele kidogo, akawaona wandugu wengine wawili, Yakobo na Yoane, waliokuwa wana wa Zebedayo. Walikuwa ndani ya chombo pamoja na baba yao Zebedayo, wakitengeneza nyavu zao. Yesu akawaita. Na mara moja wakaacha chombo pamoja na baba yao, wakamufuata Yesu. Yesu alizunguka katika Galilaya yote akifundisha katika nyumba zao za kuabudia, akihubiri Habari Njema ya Ufalme. Aliponyesha watu waliokuwa na magonjwa yote na uzaifu wa kila namna. Habari zake zikavuma katika inchi yote ya Suria. Wakamuletea watu wote walioteswa na magonjwa mbalimbali na wenye maumivu ya kila namna, wenye pepo, wenye kifafa na wenye kupooza, naye Yesu akawaponyesha. Makundi mengi ya watu yakamufuata kutoka Galilaya, inchi ya Miji Kumi, Yerusalema, Yudea, na toka ngambo ya mashariki ya muto Yordani. Yesu alipoona yale makundi ya watu, alipanda kwenye kilima. Alipokwisha kuikaa, wanafunzi wake wakamujongelea. Naye akaanza kuwafundisha akisema: “Heri wale wanaokuwa wamasikini wa roho, maana Ufalme wa mbinguni ni kwao! Heri wale wanaokuwa na huzuni, maana Mungu atawafariji! Heri wale wanaokuwa wapole, maana watarizi dunia! Heri wale wanaokuwa na njaa na kiu ya kufanya yanayokuwa haki, maana watashibishwa! Heri wale wanaokuwa na huruma, maana Mungu atawahurumia! Heri wale wanaokuwa na moyo safi, maana watamwona Mungu! Heri wale wanaoleta amani, maana wataitwa watoto wa Mungu! Heri wale wanaoteswa kwa ajili ya haki, maana Ufalme wa mbinguni ni kwao! “Heri ninyi, wakati watu wanapowatukana na kuwatesa na kuwasingizia kila namna ya ubaya kwa sababu yangu. Mufurahi na kushangilia, kwa sababu munawekewa zawadi kubwa mbinguni. Ni hivi walivyowatesa manabii walioishi mbele yenu. “Ninyi ni kama chumvi kwa watu wote. Lakini kama chumvi ikipoteza onjo lake, itatiwa nini ipate tena kukolea? Haifai tena hata kidogo, inabakilia kutupwa na kukanyagwa na watu. “Ninyi ni kama mwangaza katika dunia. Muji unaojengwa juu ya mulima hauwezi kufichama. Hakuna mutu anayewakisha taa na kuiweka chini ya kitunga, lakini anaiweka juu ya kinara kusudi iwaangazie wote wanaokuwa ndani ya nyumba. Vilevile, mwangaza wenu unapaswa kuangaza mbele ya watu, kusudi waone matendo yenu mazuri, nao wamutukuze Baba yenu anayekuwa mbinguni. “Musizani kama nilikuja kuvunja Sheria ya Musa au mafundisho ya manabii. Mimi sikukuja kuvunja, lakini kukamilisha. Kweli ninawaambia: kwa muda wote mbingu na dunia vitakapokuwa vingali, hakuna hata herufi moja wala nukta moja ya Sheria itakayoondoshwa mpaka yote yatimie. Ni kwa hiyo mutu yeyote atakayevunja hata amri moja inayokuwa ndogo kuliko zingine zote, na kuwafundisha watu wengine kufanya kama yeye, huyu atahesabiwa kuwa mudogo katika Ufalme wa mbinguni. Lakini yule atakayezishika na kuzifundisha wengine, huyu atahesabiwa kuwa mukubwa katika Ufalme wa mbinguni. Basi ninawaambia: musipokuwa wenye haki kuliko walimu wa Sheria na Wafarisayo hamutapokelewa katika Ufalme wa mbinguni. “Mumesikia kwamba babu zenu waliambiwa: ‘Usiue; mutu yeyote anayeua anapaswa kuhukumiwa.’ Lakini mimi ninawaambia: mutu yeyote anayemukasirikia ndugu yake anapaswa kuhukumiwa. Naye anayemwambia ndugu yake: ‘Hauna akili wewe!’ anapaswa kupelekwa kwenye tribinali kubwa. Naye anayemwambia: ‘Uko mwenda-wazimu!’ anastahili kutupwa katika jehenamu. Basi kama ukienda kumutolea Mungu sadaka juu ya mazabahu na pale ukikumbuka kwamba ndugu yako yuko na neno juu yako, uache sadaka yako pale mbele ya mazabahu na uende kwanza kusikilizana naye. Na kisha urudie na kutoa sadaka yako. “Kama mutu akikushitaki, upatane naye upesi wakati mungali katika njia kwenda kwenye tribinali. Kama si vile, yule anayekushitaki atakutoa kwa mwamuzi, naye mwamuzi atakupeleka kwa askari, nawe utatupwa katika kifungo. Kweli ninakuambia: hautatoka mule mpaka utakapomaliza kulipa sengi ya mwisho. “Mumesikia kwamba imesemwa: ‘Usizini.’ Lakini mimi ninawaambia: mutu yeyote anayemwangalia mwanamuke kwa kumutamani, amekwisha kuzini naye ndani ya moyo wake. Basi kama jicho lako la kuume likikukosesha, uliongoe na kulitupa mbali. Ni heri kwako kupoteza kiungo chako kimoja kuliko mwili wako wote muzima kutupwa katika jehenamu. Na kama mukono wako wa kuume ukikukosesha, uukate na kuutupa mbali. Ni heri kwako kupoteza kiungo chako kimoja kuliko mwili wako wote muzima kutupwa katika jehenamu. “Na zaidi ya hii imesemwa: ‘Kila mutu anayemufukuza muke wake amupe barua ya kuachana naye.’ Lakini mimi ninawaambia: mutu yeyote anayeachana na muke wake, isipokuwa tu kwa sababu ya uzinzi, anamufanya muke yule kuwa muzinzi kama akiolewa tena. Na mutu anayemwoa yule muke aliyefukuzwa, anazini vilevile. “Mumesikia vilevile kwamba babu zenu waliambiwa hivi: ‘Usifanye viapo vya uongo, lakini sherti utimize viapo vyako mbele ya Bwana.’ Lakini mimi ninawaambia: musiape hata kidogo kwa jina la mbingu, kwa maana ni kiti cha kifalme cha Mungu; wala kwa jina la dunia, kwa maana ni kiti chake cha kupumzishia miguu; wala kwa jina la Yerusalema, kwa maana ni muji wa Mufalme mukubwa. Mutu asiape akitaja hata kichwa chake mwenyewe, kwa maana hawezi kugeuza hata unywele wake mumoja kuwa mweupe au mweusi. Lakini munaposema, museme tu: ‘Ndiyo,’ au ‘Hapana,’ kwa maana maneno yanayosemwa zaidi ya hayo yanatoka kwa yule mwovu Shetani. “Mumesikia kwamba imesemwa hivi: ‘Jicho kwa jicho, na jino kwa jino.’ Lakini mimi ninawaambia: musirudishe mabaya kwa mabaya. Kama mutu akikupiga kofi kwa shavu la kuume, umugeuzie shavu la kushoto vilevile. Kama mutu akitaka kukushitaki kusudi akunyanganye shemizi yako, umwachie koti yako vilevile. Kama mutu anayetumwa na wakubwa akikulazimisha kubeba muzigo kilometre moja, uubebe hata kilometre mbili. Mutu akikuomba kitu, umupe. Na mutu akitaka umukopeshe, usimugeuzie mugongo. “Mumesikia kwamba imesemwa hivi: ‘Umupende mwenzako, lakini umuchukie adui yako.’ Lakini mimi ninawaambia: muwapende waadui zenu na muwaombee wale wanaowatesa. Mufanye vile kusudi mupate kuwa kweli watoto wa Baba yenu anayekuwa mbinguni. Kwa maana yeye anawaangazia waovu na wema jua lake, naye anawanyeshea mvua wenye haki na wasiokuwa wenye haki. Zawadi gani mutapata kutoka kwa Mungu, kama mukiwapenda tu wenye kuwapenda? Hata walipishaji wa kodi wanaokuwa wakorofi wanatendeana vile! Na kama mukiwasalimia wandugu zenu tu, munatenda tendo gani la kupita wengine? Hata wapagani wanatendeana vile! Basi mukuwe wakamilifu, kama vile Baba yenu wa mbinguni anavyokuwa mukamilifu. “Mujiangalie musifanye matendo mema mbele ya watu kusudi mujionyeshe kwao. Kwa maana mukifanya hivi hamutapata faida kutoka kwa Baba yenu anayekuwa mbinguni. “Basi wakati unapomusaidia masikini, usipige baragumu, kama vile wanafiki wanavyofanya katika nyumba za kuabudia na katika barabara kusudi wasifiwe na watu. Kweli ninawaambia: wamekwisha kupata faida yao. Lakini wewe, unapomusaidia masikini, ufanye tendo lile kwa uficho hata rafiki yako wa kweli asijue. Hivi tendo lile halitatoka inje, naye Baba yako anayeona tendo unalofanya kwa siri, atakulipa. “Munapoomba, musikuwe kama wanafiki, kwa maana wanapenda kuomba wakisimama katika nyumba za kuabudia na pembeni ya barabara, kusudi wapate kujionyesha mbele ya watu. Kweli ninawaambia: wamekwisha kupata faida yao. Lakini wewe, unapoomba, ingia ndani ya chumba chako, funga mulango na uombe kwa Baba yako asiyeonekana. Na Baba yako anayeona tendo unalofanya kwa siri, atakulipa. “Tena munapoomba, musitumie maneno mengi yasiokuwa na maana kama vile wapagani wanavyofanya, kwa sababu wanawaza kama Mungu atawasikia kama wakisema maneno mengi. Basi musifanye kama wao, musifanane nao kwa maana Baba yenu anajua vitu munavyohitaji mbele hamujamwomba. Basi muangalie namna munavyopaswa kusema munapoomba: ‘Baba yetu unayekuwa mbinguni, Jina lako litukuzwe; Ufalme wako ukuje; mapenzi yako yafanyike katika dunia kama inavyokuwa mbinguni. Utupe chakula chetu cha kila siku. Utusamehe makosa yetu, kama sisi tunavyowasamehe wanaotukosea, Usituache kuanguka katika majaribu, lakini utuokoe na yule Mwovu. [Kwa maana ufalme, uwezo na utukufu ni vyako hata milele. Amina.]’ “Hivi, mukiwasamehe watu wengine makosa wanayowatendea, Baba yenu anayekuwa mbinguni atawasamehe vilevile. Lakini kama musipowasamehe wengine wanaowakosea, Baba yenu hatawasamehe makosa yenu vilevile. “Munapofunga kula chakula, musifanye kama wanafiki, wanaojigeuza kuwa wenye sikitiko na kukunja nyuso zao, kusudi watu waone kwamba wanafunga. Kweli ninawaambia: wamekwisha kupata faida yao. Lakini wewe unapofunga kula chakula, unawe uso wako na kuchanua nywele zako, kusudi usijionyeshe kwa watu kwamba unafunga. Jambo hilo litajulikana tu kwa Baba yako anayekuwa kwa siri. Naye Baba yako anayeona tendo unalofanya kwa siri, atakulipa. “Musijiwekee akiba katika dunia hii, pahali nondo na kutu vinapoharibu, nao wizi wanapotoboa nyumba na kuiba. Lakini mujiwekee akiba katika mbingu, pahali nondo wala kutu visipoweza kuharibu, nao wizi wasipoweza kutoboa na kuiba. Kwa maana pahali akiba yako inapokuwa, ni pale roho yako inapokuwa vilevile. “Macho ni taa ya mwili. Kama macho yako yakiwa mazima, mwili wako wote utabaki katika mwangaza. Lakini kama macho yako yanaharibika, mwili wako wote utabaki katika giza. Basi ikiwa mwangaza unaokuwa ndani yako umegeuka kuwa giza, giza hilo ni nzito sana! “Hakuna mutu anayeweza kuwatumikia wabwana wawili. Kwa maana atamuchukia mumoja na kumupenda mwingine; au atashikamana na mumoja na kumuzarau mwingine. Hamuwezi kutumikia Mungu na kutumikia mali vilevile. “Ni kwa sababu hii ninawaambia ninyi: musijisumbue kwa ajili ya maisha yenu, kwa ajili ya chakula au kwa ajili ya kinywaji, wala musijisumbue kwa ajili ya miili yenu kwamba mutavaa nini. Uzima ni wa lazima kuliko vyakula, nao mwili ni wa lazima kuliko nguo. Muangalie ndege wanaoruka katika anga: wao hawapandi mbegu wala hawavuni, wala hawaweki mavuno ndani ya gala, lakini Baba yenu anayekuwa mbinguni anawakulisha! Basi ninyi si wa lazima zaidi kuliko ndege wale? Nani kati yenu, kwa ajili ya kujisumbua kwake, anaweza kujiongezea hata siku moja kupita muda wa maisha yake? “Kwa sababu gani munajisumbua kwa ajili ya nguo? Muangalie maua jinsi yanavyoota. Hayatumiki wala kujisukia nguo. Lakini ninawaambia kwamba hata mufalme Solomono katika utukufu wote aliokuwa nao hakuvaa nguo inayoweza kulinganishwa na uzuri wa moja la maua yale. Basi ikiwa Mungu anavalisha majani kama hivi, yanayoonekana leo na kesho yanatoweka na kutupwa katika moto, hatawavalisha ninyi vizuri zaidi, ninyi wenye imani ndogo? “Basi musijisumbue kwa ajili ya chakula, kwa ajili ya kinywaji au kwa ajili ya nguo. Ni wapagani ndio wanaoshugulika kwa kutafuta vitu vile vyote. Baba yenu anayekuwa mbinguni anajua kama munahitaji vitu vile vyote. Lakini ninyi mushugulikie kwanza Ufalme wa Mungu na kufuata haki mbele yake, naye atawaongezea vitu vile vyote. Basi musijisumbue kwa ajili ya kesho, kwa maana kesho itajisumbukia yenyewe. Kila siku ina masumbuko yake inayoitoshelea. “Musiwahukumu wengine kusudi Mungu asiwahukumu ninyi vilevile. Kwa maana mutahukumiwa kufuatana na namna munavyowahukumu wengine, na kipimo kile munachowapimia wengine ndicho kitakachotumiwa kwenu vilevile. Namna gani unaona vumbi inayokuwa ndani ya jicho la ndugu yako, lakini haufikiri juu ya nguzo inayokuwa ndani ya jicho lako? Au namna gani unaweza kumwambia ndugu yako kwamba aache umwondoe vumbi inayokuwa ndani ya jicho lake, wakati ndani ya jicho lako mwenyewe mungali ile nguzo? Wewe munafiki, ondosha kwanza nguzo kutoka ndani ya jicho lako, kisha utaweza kuona waziwazi na kuweza kuondoa ile vumbi inayokuwa ndani ya jicho la ndugu yako. “Musiwape imbwa vitu vitakatifu, kusudi wasiwageukie na kuwararua, wala musiwatupie nguruwe ushanga zenu za bei kusudi wasizikanyagekanyage. “Muombe, nanyi mutapewa; mutafute, nanyi mutapata; mupige hodi, nanyi mutafunguliwa mulango. Kwa maana kila mutu anayeomba, anapewa; naye anayetafuta, anapata, naye anayepiga hodi, anafunguliwa. Ni nani kati yenu anayeweza kumupa mutoto wake jiwe kama akimwomba mukate? Au nani anaweza kumupa nyoka kama akimwomba samaki? Basi ikiwa ninyi munaokuwa waovu munajua kuwapa watoto wenu vitu vizuri, zaidi sana Baba yenu anayekuwa mbinguni atawapa wale wanaomwomba vitu vizuri zaidi. “Basi jambo lolote munalotaka wengine wawatendee, ninyi mulitende kwao vilevile, kwa maana kile ndicho kifungo cha Sheria ya Musa na mafundisho ya manabii. “Muingie kwa kupitia mulango unaokuwa mwembamba. Kwa maana njia inayoongoza kufikia kwenye lufu ni kubwa, nao mulango unaoiingilia ni mupana, nao watu wanaoipitia ni wengi. Lakini njia inayoongoza kufikia kwenye uzima ni yenye kusongamana na mulango unaoiingilia ni mwembamba, nao watu wanaoifuata ni wachache tu. “Mufanye angalisho na manabii wa uongo; kwa maana wanakuja kwenu wakionekana kwa inje kama vile kondoo, lakini ndani, wao ni kama imbwa wakali wa pori. Mutawatambua kwa matendo yao. Watu hawachumi matunda ya mizabibu au ya tini toka juu ya miti ya miiba. Na ni vile inavyokuwa: kila muti muzuri unazaa matunda mazuri, lakini kila muti mubaya unazaa matunda mabaya. Muti muzuri hauwezi kutoa matunda mabaya, wala muti mubaya hauwezi kutoa matunda mazuri. Kila muti usiozaa matunda mazuri unakatwa na kutupwa katika moto. Basi kwa hiyo, mutawatambua manabii wa uongo kwa njia ya matendo yao. “Si kila mutu anayeniita ‘Bwana, Bwana,’ atakayeingia katika Ufalme wa mbinguni, lakini yule tu anayefanya mapenzi ya Baba yangu anayekuwa mbinguni. Siku ile ya hukumu itakapotimia, wengi wataniambia: ‘Bwana, Bwana, sisi hatukutangaza ujumbe wa Mungu? Nasi hatukufukuza pepo kwa jina lako na kufanya maajabu mengi kwa jina lako?’ Halafu mimi nitawaambia hivi waziwazi: ‘Sikuwajua ninyi hata siku moja. Mutoke karibu nami, ninyi watenda maovu.’ “Basi kila mutu anayesikia hayo maneno yangu na kuyashika, anafananishwa na mutu mwenye akili aliyejenga nyumba yake juu ya jiwe. Mvua ikanyesha, mito ikajaa, nao upepo ukavuma na kuishambulia nyumba ile, lakini haikuanguka, kwa sababu musingi wake ulikuwa umejengwa juu ya jiwe. “Lakini kila mutu anayesikia maneno ninayotoka kusema bila kuyashika, anafananishwa na mutu mupumbafu aliyejenga nyumba yake juu ya udongo wenye kichanga. Mvua ikanyesha, mito ikajaa, upepo ukavuma na kupiga nyumba ile, nayo ikaanguka na kubomoka kabisa.” Yesu alipomaliza kusema maneno hayo, makundi ya watu wakashangaa sana kwa kuona namna alivyowafundisha; kwa maana hakuwafundisha sawa vile walimu wao wa Sheria, lakini kama vile mutu mwenye mamlaka. Yesu aliposhuka toka kwa mulima, makundi mengi ya watu wakamufuata. Halafu mutu mumoja mwenye ukoma akakuja, akapiga magoti mbele yake na kumwambia: “Bwana, kama ukitaka, unaweza kunitakasa.” Yesu akanyoosha mukono, akamugusa na kumwambia: “Ninataka, utakaswe!” Na mara moja mutu yule akatakaswa ukoma wake. Kisha Yesu akamwambia: “Angalisho, usimwambie mutu neno juu ya hii. Lakini kwenda na kumwonyesha kuhani jinsi unavyokuwa sasa. Kisha utoe sadaka kama Musa alivyoamuru, kuwa ushuhuda kwa watu wote kwamba umetakaswa.” Yesu alipokuwa akiingia katika muji Kapernaumu, mukubwa mumoja wa waaskari akamufikia na kumusihi, akisema: “Bwana, mutumishi wangu anawezwa na ugonjwa wa kupooza, naye amelala ndani ya nyumba, akiteswa sana.” Yesu akamwambia: “Nitakuja kumuponyesha.” Lakini yule mukubwa akamujibu: “Bwana, mimi sistahili kukupokea ndani ya nyumba yangu. Lakini uamuru kwa neno tu na mutumishi wangu atapona. Hata mimi vilevile ni mutu mwenye kuwa chini ya mamlaka ya wakubwa, na tena nina waaskari wengine wanaokuwa chini yangu. Nami nikimwambia mumoja: ‘Kwenda!’, naye anakwenda. Nikimwambia mwingine: ‘Kuja!’, naye anakuja. Na nikimwambia mutumishi wangu: ‘Fanya hivi!’, naye anafanya vile.” Yesu aliposikia maneno haya, akashangaa na kuwaambia watu waliomufuata: “Kweli ninawaambia: katika inchi yote ya Israeli, sijaona bado mutu anayekuwa na imani kubwa kama huyu. Ninawaambia wazi kwamba watu wengi watakuja toka mashariki na magaribi, nao watachangia meza pamoja na Abrahamu, Isaka, na Yakobo kwenye karamu katika Ufalme wa mbinguni. Lakini wale waliopaswa kushiriki katika Ufalme ule watatupwa inje kwenye giza, na kule watalia na kusaga meno.” Kisha Yesu akamwambia yule mukubwa wa waaskari hivi: “Urudie kwako, na ifanyike kwako sawa ulivyoamini.” Na saa ile ile mutumishi wake akapona. Kisha Yesu akafika kwa nyumba ya Petro, na mule akamukuta mama mukwe wa Petro amelala katika kitanda na ugonjwa wa homa. Yesu akamugusa mukono, naye akapona homa. Halafu mama yule akasimama na kuanza kumushugulikia. Na ilipokuwa magaribi, wakamuletea Yesu watu wengi waliokuwa na pepo. Naye akawafukuza wale pepo akiwaamuru kwa neno tu na kuwaponyesha wagonjwa wote. Alifanya hivi kusudi yatimie maneno yaliyosemwa kwa njia ya nabii Isaya: “Yeye alitwaa uzaifu wetu, naye amebeba muzigo wa magonjwa yetu.” Yesu alipoona kundi la watu wakimuzunguka, akatoa amri ya kuvuka ngambo ingine ya ziwa. Mwalimu mumoja wa Sheria akamufikia na kumwambia: “Mwalimu, nitakufuata popote utakapokwenda.” Yesu akamujibu: “Mbweha wako na makao yao ndani ya matundu, nao ndege wako na chicha, lakini Mwana wa Mutu hana nafasi ya kulala.” Na mutu mwingine mumoja kati ya wanafunzi wake akamwambia: “Bwana, unipe ruhusa kwanza niende kuzika baba yangu.” Lakini Yesu akamujibu: “Unifuate mimi, uwaache hao wafu wazike wafu wao.” Halafu Yesu akaingia ndani ya chombo, nao wanafunzi wake wakaenda naye. Mara moja zoruba kubwa ikatokea katika ziwa na maji yakajitupatupa ndani ya chombo. Lakini Yesu alikuwa amelala usingizi. Wanafunzi wake wakamujongelea, wakamwamusha na kumwambia: “Bwana, utuokoe! Tunakufa!” Yesu akawajibu: “Sababu gani munaogopa kama hivi? Hakika imani yenu ni ndogo!” Halafu akasimama, akakaripia zoruba na maji na kukakuwa kimya kabisa ndani ya ziwa. Nao wakashangaa, wakisema: “Huyu ni mutu gani, hata zoruba na ziwa vinamutii?” Yesu alipofika ngambo ingine ya ziwa la Galilaya, katika inchi ya Wagedari, watu wawili wenye pepo wakamufikia, wakitoka kwenye makaburi. Watu wale walikuwa na pepo wakali sana, hata hakuna mutu aliyesubutu kupita katika njia ile. Halafu wakaanza kulalamika wakisema: “Kuna maneno gani kati yako na sisi wewe Mwana wa Mungu? Umekuja hapa kwa kututesa mbele ya kutimia kwa wakati wetu?” Na karibu na pale kulikuwa kundi kubwa la nguruwe wakijitafutia chakula. Wale pepo wakamusihi Yesu wakisema: “Ikiwa unataka kutufukuza, ututume tuingie ndani ya wale nguruwe.” Na Yesu akawaambia: “Mwende!” Basi wakatoka ndani ya wale watu na kuingia ndani ya nguruwe. Mara moja kundi zima likatelemuka mbio toka kwenye maporomoko ya mulima na kujitupa ndani ya ziwa nao wakazama ndani ya maji. Wachungaji wa nguruwe wale wakaenda mbio katika muji kupasha habari za mambo yaliyotendeka na habari ya wale watu wawili waliokuwa na pepo. Basi watu wote wa muji wakatoka kwa kumufikia Yesu na wakati walipomwona wakamusihi aondoke katika inchi yao. Yesu akaingia katika chombo akavuka tena ziwa kwenda upande wa magaribi, naye akafika katika muji wake. Na kule wakamuletea mutu mwenye ugonjwa wa kupooza, akilala juu ya kipoyi. Yesu alipoona namna watu wale walivyomwaminia, akamwambia yule mwenye kupooza: “Mutoto wangu, ujipe moyo! Zambi zako zimesamehewa!” Halafu walimu wamoja wa Sheria waliokuwa pale wakajisemesha: “Mutu huyu anamutukana Mungu!” Naye Yesu akijua mafikiri yao, akawauliza: “Sababu gani munawaza maneno hayo mabaya? Kitu gani kinachokuwa chepesi kusema: ‘Zambi zako zimesamehewa’, au kusema: ‘Simama, utembee’? Basi, ninataka mujue kwamba Mwana wa Mutu yuko na mamlaka ya kusamehe zambi hapa katika dunia.” Kwa hiyo akamwambia yule mutu mwenye kupooza: “Simama, utwae kipoyi chako na uende kwako.” Na mutu yule akasimama na kwenda kwake. Watu walipoona jambo hilo wakaogopa na kumusifu Mungu aliyewapa watu mamlaka ya namna ile. Yesu alipokuwa akipita, akamwona mutu anayeitwa Matayo, akiikaa katika nyumba ya kulipishia kodi. Yesu akamwambia: “Unifuate!” Naye akasimama na kumufuata. Nyuma Yesu akaikaa kula chakula ndani ya nyumba ya Matayo. Walipishaji wengi wa kodi na watenda mabaya wengine walikuwa wamekuja pale, nao waliikaa kula pamoja na Yesu na wanafunzi wake. Nao Wafarisayo walipoona mambo hayo, wakawaambia wanafunzi wake: “Kwa sababu gani mwalimu wenu anakula pamoja na walipishaji wa kodi na watenda mabaya?” Lakini Yesu alisikia vile walivyosema, na kwa hiyo akawaambia: “Wenye afya nzuri hawahitaji muganga lakini wale wanaokuwa wagonjwa. Muende kujifunza maana ya Maandiko Matakatifu yanayosema: ‘Ninataka huruma, lakini si sadaka zenu.’ Kwa maana sikukuja kuwaita wenye haki kunifuata, lakini watenda mabaya.” Wanafunzi wa Yoane Mubatizaji wakamufikia Yesu na kumwuliza: “Sababu gani sisi na Wafarisayo tunafunga kula chakula, lakini wanafunzi wako hawafungi?” Yesu akawajibu: “Munafikiri kwamba warafiki za bwana-arusi wanaweza kufanya kilio wakati bwana-arusi angali pamoja nao? Hapana! Lakini kutakuwa siku bwana-arusi atakapoondoshwa kati yao; ni siku zile watafunga kula. “Hakuna mutu anayeshonea kiraka kipya juu ya nguo ya zamani. Kama anafanya vile, kile kiraka kipya kinapasua nguo ya zamani, na kupasuka kwake kunaongezeka zaidi. Vilevile hawatii divai mupya ndani ya machupa ya ngozi yenye kuzeeka. Wakifanya vile yale machupa yanapasuka, halafu divai inamwangika, nayo machupa yanapotea bure. Lakini inafaa kutia divai mupya ndani ya machupa mapya ya ngozi, navyo vyote vinalindwa vizuri.” Yesu alipokuwa hajamaliza kusema maneno hayo, mukubwa mumoja akafika, akapiga magoti mbele yake na kumwambia: “Binti yangu anakufa sasa hivi; lakini kuja, uweke mikono yako juu yake kusudi apate kufufuka.” Halafu Yesu akaondoka, akamufuata pamoja na wanafunzi wake. Na kulikuwa mwanamuke mumoja mwenye ugonjwa wa kutokwa na damu kwa muda wa miaka kumi na miwili. Yeye akakuja nyuma ya Yesu na kugusa upindo wa nguo yake, kwa maana alikuwa akijisemesha: “Kama nikigusa tu nguo yake, nitapona.” Naye Yesu alipogeuka, akamwona na kumwambia: “Binti yangu, ujipe moyo! Imani yako imekuponyesha.” Na mwanamuke yule akapona saa ile ile. Yesu alipofika kwa nyumba ya yule mukubwa, akaona wapiga muziki wakiimba nyimbo za kilio nalo kundi la watu wakifanya kelele. Halafu akasema: “Mutoke hapa. Binti huyu mudogo hakukufa, lakini analala tu.” Nao wakaanza kumuchekelea. Na watu wale walipokwisha kufukuzwa, Yesu akaingia ndani ya chumba, akashika mukono wa yule binti, naye akasimama. Habari za jambo hili zikaenea katika inchi ile yote. Yesu akaondoka toka pale, naye alipokuwa katika njia, vipofu wawili wakamufuata wakilalamika, wakisema: “Utuhurumie, Ee Mwana wa Daudi!” Na wakati Yesu alipoingia ndani ya nyumba, wale vipofu wakamufikia. Naye akawauliza: “Munaamini kwamba ninaweza kuwafanyia jambo hilo?” Nao wakamujibu: “Ndiyo, Bwana.” Halafu Yesu akagusa macho yao, akisema: “Ifanyike kwenu sawa vile munavyoaminia.” Nayo macho yao yakapona. Na Yesu akawaagiza kwa nguvu, akisema: “Angalisho, musimujulishe hata mutu mumoja jambo hili.” Lakini wakaenda na kuanza kutangaza habari za Yesu katika inchi ile yote. Watu hao wawili walipokwisha kwenda, wakamuletea Yesu mutu mumoja bubu aliyeshikwa na pepo. Wakati Yesu alipokwisha kumufukuza yule pepo, yule bubu akaanza kusema. Nao watu wote wakashangaa na kusema: “Hatujaona jambo kama hili katika inchi yote ya Israeli!” Lakini Wafarisayo wakasema: “Ni mukubwa wa pepo ndiye anayemupa uwezo wa kufukuza pepo.” Yesu alizunguka katika miji na vijiji vyote, akiwafundisha watu katika nyumba zao za kuabudia, akiwahubiri Habari Njema ya Ufalme. Aliponyesha magonjwa yote na uzaifu wa kila namna. Yesu alipoona kundi la watu, aliwasikilia huruma, kwa maana walikuwa wamesumbuka na kuregea, kama kondoo wasiokuwa na muchungaji. Halafu akawaambia wanafunzi wake: “Mavuno ni mengi, lakini wavunaji ni wachache. Basi muombe Bwana mwenyeji wa mavuno awatume wavunaji wengine kwa kuvuna mavuno yake.” Yesu akawaita wanafunzi wake kumi na wawili na akawapa mamlaka ya kufukuza pepo na kuponyesha magonjwa yote na uzaifu wa kila namna. Na haya ndiyo majina ya hao mitume wake kumi na wawili: kwanza Simoni (anayeitwa vilevile Petro) na ndugu yake Andrea; Yakobo na ndugu yake Yoane, ambao ni wana wa Zebedayo; kisha Filipo na Bartolomayo, Toma na Matayo aliyekuwa mulipishaji wa kodi; Yakobo mwana wa Alfayo, na Tadeo; Simoni wa kundi la Wazeloti, na Yuda Iskariota aliyemutoa Yesu. Hao ndio wanafunzi kumi na wawili Yesu aliowatuma, akiwaagiza mambo haya: “Musiende katika inchi za watu wa mataifa mengine wala musiingie katika muji wowote wa Samaria. Lakini muwaendee wandugu zenu wa inchi ya Israeli, wanaokuwa kama kondoo wanaopotea. Mutakapokuwa mukienda, muhubiri kwa watu kwamba Ufalme wa mbinguni umekaribia! Muponyeshe wagonjwa, mufufue wafu, mutakase wenye ukoma, mufukuze pepo. Mulipokea bure, mutoe bure vilevile. Musibebe zahabu, wala feza, wala vikoroti vya shaba ndani ya mikaba yenu. Vilevile musibebe mifuko, kanzu mbili, viatu wala fimbo, kwa sababu mutumishi anastahili kupewa posho lake. “Mutakapoingia katika muji au katika kijiji, mutafute mutu anayekuwa tayari kwa kuwakaribisha, nanyi mukae kwake mpaka mutakapotoka kule. Mutakapoingia ndani ya nyumba, muwasalimie watu wanaokuwa mule, mukisema: ‘Amani kwenu.’ Kama watu wa nyumba ile wakiwakaribisha, wakuwe na amani ile muliyowatakia, lakini wasipowakaribisha, amani ile iwarudilie. Na katika nyumba au muji wowote watakapokataa kuwakaribisha na kukataa kusikiliza maneno yenu, mutakapotoka kule mukungute mavumbi toka juu ya miguu yenu. Kweli ninawaambia: kwa Siku ya hukumu, watu wa muji ule wataazibiwa vikali zaidi kuliko watu wa muji wa Sodoma na wa Gomora. “Muangalie! Ninawatuma kama kondoo katikati ya imbwa wa pori. Basi mukuwe waangalifu kama nyoka na wakamilifu kama njiwa. Mujilinde, kwa maana watu watawapeleka mbele ya tribinali kubwa nao watawapiga fimbo ndani ya nyumba zao za kuabudia. Vilevile mutapelekwa mbele ya wakubwa na wafalme kwa ajili yangu, kusudi mutoe ushuhuda wangu mbele yao na mbele ya watu wa mataifa mengine. Lakini watakapowapeleka kwa kuhukumiwa, musijihangaishe juu ya maneno mutakayoyasema wala juu ya namna mutakavyosema, kwa maana saa ile ile mutapewa maneno mutakayoyasema. Maneno mutakayoyasema hayatatoka kwenu, lakini yatatoka kwa Roho wa Baba wenu Mungu atakayesema ndani yenu. “Ndugu atamutoa ndugu, kusudi auawe, na baba atamutoa mutoto wake, nao watoto watawageukia wazazi wao na kuwaua. Na watu wote watawachukia kwa ajili yangu. Lakini atakayevumilia mpaka mwisho ataokolewa. Watakapowatesa katika muji mumoja, mukimbilie katika muji mwingine. Kweli ninawaambia: hamutamaliza kuzunguka katika miji yote ya Israeli mbele ya kurudi kwa Mwana wa Mutu. “Mwanafunzi hamupiti mwalimu wake, wala mutumishi hamupiti bwana wake. Lakini inatosha kwa mwanafunzi kufanana na mwalimu wake na mutumishi kufanana na bwana wake. Ikiwa wanamwita mukubwa wa jamaa Belzebuli, hawatakosa kuwaita watu wa jamaa yake kwa majina mabaya zaidi. “Basi musiwaogope watu wale. Hakuna kitu chochote kinachofichwa kitakachokosa kuvumbulikana wala hakuna siri itakayokosa kujulikana. Neno ninalowaambia katika giza, muliseme muchana kati. Vilevile neno munalosikia kwa siri, mulitangaze mukisimama juu ya paa ya nyumba. Musiwaogope wale wanaoweza kuua tu mwili, lakini wasioweza kuua roho. Lakini zaidi mumwogope Mungu anayeweza kuharibu mwili pamoja na roho katika jehenamu. Ndege wawili wadogo wanauzishwa kwa bei chini kabisa. Ingawa vile hakuna hata mumoja wao anayekufa bila mapenzi ya Baba yenu. Na kwa upande wenu, yeye anajua hesabu ya nywele zote za vichwa vyenu. Basi musiogope, kwa sababu ninyi ni bora zaidi kuliko kundi la ndege wengi! “Kila mutu anayenikubali mbele ya watu, nami nitamukubali vilevile mbele ya Baba yangu anayekuwa mbinguni. Lakini kila mutu anayenikana mbele ya watu, nami nitamukana vilevile mbele ya Baba yangu anayekuwa mbinguni. “Musifikiri kwamba nimekuja kuleta amani katika dunia. Mimi sikukuja kuleta amani, lakini upanga. Kwa maana nimekuja kuleta matengano kati ya mutu na baba yake, kati ya binti na mama yake, kati ya mukwe na mama mukwe; na adui wa mutu atakuwa wa jamaa yake mwenyewe. “Yeye anayemupenda baba yake au mama yake kuliko mimi, hastahili kuwa wangu, na yeyote anayemupenda mwana wake au binti yake kuliko mimi hastahili kuwa wangu vilevile. Naye asiyejitolea kwa kubeba musalaba wake na kunifuata hastahili kuwa wangu. Kwa maana mutu anayetaka kulinda uzima wake, ataupoteza; lakini yule atakayetoa uzima wake kwa ajili yangu, ataupata tena. “Mutu anayewapokea ninyi, ananipokea mimi; naye anayenipokea, anamupokea yule aliyenituma. Yule anayemupokea nabii wa Mungu, kwa sababu ni nabii, atapokea zawadi sawa nabii yule. Vilevile yule anayemupokea mwenye haki, kwa sababu ni mwenye haki, atapokea zawadi sawa yule mwenye haki. Na yeyote atakayetoa hata kikombe kimoja tu cha maji ya baridi kwa mumoja wa hao wanaokuwa wadogo kati ya wanafunzi wangu, kwa sababu yeye ni mwanafunzi wangu, kweli ninawaambia: mutu yule hatakosa kupewa zawadi yake.” Yesu alipomaliza kutoa maagizo hayo kwa wanafunzi wake kumi na wawili, akaondoka kule, akaenda kufundisha na kuhubiri katika miji ya inchi ile. Yoane Mubatizaji, akiwa katika kifungo, akapata habari za mambo Kristo aliyokuwa akifanya. Basi akawatuma wanafunzi wake kumwuliza Yesu: “Wewe ndiwe yule aliyepaswa kuja kutuokoa au tumungojee mwingine?” Yesu akawajibu: “Mwende kumwelezea Yoane mambo munayosikia na kuyaona: vipofu wanapata kuona, viwete wanatembea, wenye ukoma wanatakaswa, viziwi wanapata kusikia, wafu wanafufuliwa na Habari Njema inahubiriwa kwa wamasikini. Heri mutu yule mimi sitakayekuwa kikwazo kwake!” Wale wanafunzi wa Yoane walipoondoka, Yesu akaanza kuwaambia makundi ya watu habari za Yoane: “Mulienda katika jangwa kwa kuangalia nini? Tete linalotikiswa na upepo? Hapana! Basi mulienda kuona nini? Mutu aliyevaa nguo nzuri? Hapana! Wale wanaovaa nguo nzuri wanakaa katika nyumba za wafalme. Basi mulikwenda kuona nini? Nabii? Ndiyo, ninawaambia, yeye ni mukubwa kupita hata nabii. Huyu ndiye maneno haya yameandikwa juu yake katika Maandiko Matakatifu: ‘Ninamutuma mujumbe wangu akutangulie, kusudi akutengenezee njia utakayopitia!’ “Kweli ninawaambia: kati ya watu wanaoishi katika dunia, hakuna mutu anayekuwa mukubwa kuliko Yoane Mubatizaji. Lakini yeyote anayeonekana kuwa mudogo katika Ufalme wa mbinguni anahesabiwa kuwa mukubwa kuliko yeye. Tangia wakati Yoane Mubatizaji alipohubiri mpaka sasa, watu wanapinga Ufalme wa mbinguni, nao watu wakali wanajaribu kuukamata kwa kinguvu. Kwa maana mambo hayo yalitangazwa na manabii wote na Sheria ya Musa mpaka wakati wa Yoane. Na ikiwa munasadiki, Yoane ndiye nabii Elia aliyepaswa kuja. Mwenye kuwa na masikio ya kusikia, asikie! “Nitawafananisha watu wa kizazi hiki na nini? Wanafanana na watoto wanaoikaa kwenye nafasi ya makutano na kuita wenzao wakisema: ‘Tuliwapigia ngoma, lakini hamukucheza! Tuliimba wimbo wa kilio, lakini hamukulia!’ Kwa maana Yoane alikuja, alifunga kula chakula na kunywa, nao wakasema: ‘Yuko na pepo!’ Mwana wa Mutu alikuja, yeye anakula na kunywa, nao wanasema: ‘Angalia huyu mulafi na mulevi, rafiki wa walipishaji wa kodi na watenda maovu wenzao.’ Lakini hekima ya Mungu ilionyeshwa kuwa ya haki kwa njia ya matendo yake.” Kisha Yesu akaanza kuonya miji ambamo alifanya miujiza mingi zaidi, kwa sababu wakaaji wa kule hawakugeuka toka zambi zao. Akasema: “Ole kwako, muji Korazini! Ole kwako, muji Betesaida! Kwa maana miujiza iliyofanyika ndani yenu ingalifanyika katika muji wa Tiro na muji wa Sidona, wakaaji wa kule wangekwisha zamani kuvaa magunia na kujipakaa majivu, kwa kuonyesha kwamba wamegeuka toka zambi zao. Kwa hiyo ninawaambia kwamba kwa Siku ya hukumu, ninyi mutaazibiwa zaidi kuliko muji wa Tiro na wa Sidona. Nawe, muji Kapernaumu, unafikiri kwamba utapandishwa mpaka juu mbinguni? Utashushwa mpaka chini katika kuzimu. Kwa maana miujiza iliyofanyika ndani yako ingalifanyika katika Sodoma, muji ule ungekuwa ungali hata leo. Kwa hiyo ninawaambia kwamba kwa Siku ya hukumu, wewe utaazibiwa zaidi kuliko watu wa Sodoma!” Katika siku zile Yesu akasema: “Ee Baba, Mwenyeji wa mbingu na dunia, ninakushukuru kwa maana mambo uliyoyaficha kwa watu wenye hekima na elimu, umeyafunua kwa wanaokuwa wadogo. Ndiyo, Baba, hayo yote ni kutokana na mapenzi yako. “Baba yangu ameweka vitu vyote katika mikono yangu. Hakuna mutu anayemujua Mwana isipokuwa Baba, wala hakuna anayemujua Baba isipokuwa Mwana, na yeyote Mwana anayetaka kumujulisha kwake. “Mukuje kwangu ninyi wote munaosumbuka na kulemewa na mizigo mizito, nami nitawapumzisha. Mukubali kuongozwa nami kama vile ngombe dume anayefungiwa nira, nanyi mufuate mafundisho yangu maana mimi ni mupole na munyenyekevu. Kwa hiyo mutapumzika. Nira yangu si nzito, nao muzigo nitakaowabebesha ni mwepesi.” Katika siku zile Yesu akapita katika mashamba ya ngano kwa siku moja ya Sabato. Wanafunzi wake wakasikia njaa; kwa hiyo wakaanza kuchumachuma masuke ya ngano na kuyakula. Wafarisayo walipoona mambo hayo, wakamwambia Yesu: “Angalia! Wanafunzi wako wanafanya mambo yanayokatazwa kufanya kwa siku ya Sabato!” Yesu akawajibu: “Hamujasoma bado vile Daudi alivyofanya wakati yeye pamoja na watu wake waliposikia njaa? Aliingia ndani ya nyumba ya Mungu na kula mikate mitakatifu iliyotolewa kwa Mungu. Ijapokuwa vile haikuruhusiwa kwake wala kwa watu wake kukula mikate kama ile, isipokuwa makuhani peke yao. Vilevile hamujasoma bado katika kitabu cha Sheria ya Musa kwamba kila siku ya Sabato, makuhani wanaotumika ndani ya hekalu wanavunja Sheria inayoelekea siku ile, nao hawahesabiwi kuwa na kosa? Lakini sasa ninawaambia kama hapa kuna mukubwa kupita hekalu! Mungejua maana ya Maandiko haya Matakatifu, yanayosema: ‘Ninataka huruma, lakini si sadaka zenu,’ hamungehukumu watu hawa wasiokuwa na kosa. Kwa maana Mwana wa Mutu ndiye Bwana wa siku ya Sabato.” Yesu akaondoka ngambo za kule, na kwenda ndani ya nyumba moja ya kuabudia. Mule ndani mulikuwa mutu mumoja mwenye mukono unaokauka. Nao watu wamoja waliokuwa pale walitafuta sababu ya kumushitaki Yesu; kwa hiyo wakamwuliza: “Sheria yetu inaruhusu kumuponyesha mutu kwa siku ya Sabato?” Yesu akawajibu: “Kama mutu mumoja kati yenu akiwa na kondoo mumoja, na kondoo yule akitumbukia ndani ya shimo kwa siku ya Sabato, hatamukamata na kumwondosha mule siku ile ile? Naye mutu ni wa lazima kuliko kondoo! Basi Sheria inaturuhusu kutenda mema kwa siku ya Sabato.” Kisha Yesu akamwambia yule mutu: “Nyoosha mukono wako.” Naye akaunyoosha, nao ukakuwa tena muzima sawa ule mwingine. Wafarisayo wakaondoka pale na kwenda kufanya shauri la kumwua Yesu. Yesu alipojua habari ile, akaondoka kule. Watu wengi wakamufuata, naye akawaponyesha wagonjwa wote. Akawaagiza wasimutambulishe kwa watu. Ilitokea vile kusudi yatimie maneno haya Mungu aliyoyasema kwa njia ya nabii Isaya: “Muangalie, mutumishi wangu niliyejichagulia, anayekuwa mupendwa wangu, ninayependezwa naye. Nitamujaza Roho wangu, naye atatangaza haki yangu kwa mataifa. Hatabishana wala kupiga kelele, wala hakuna atakayesikia sauti yake katika barabara. Hatavunja tete linalokunja, wala hatazimisha taa inayofifia, mpaka aiwezeshe haki kutawala. Nayo mataifa yote yatamutumainia.” Kisha wakamuletea Yesu mutu mumoja aliyeshikwa na pepo, aliyemufanya kuwa kipofu na bubu. Yesu akamuponyesha mutu yule hata akaanza kusema na kuona. Na kundi lote la watu waliokuwa pale wakashangaa na kusema: “Huyu anaweza kuwa kweli Mwana wa Daudi?” Lakini wakati Wafarisayo waliposikia maneno yale, wakasema: “Ni Belzebuli, mukubwa wa pepo ndiye anayemupa mutu huyu uwezo wa kufukuza pepo.” Yesu akitambua mafikiri yao, akawaambia: “Watu wa ufalme wowote wakigombana wao kwa wao, ufalme ule utaanguka. Nao wakaaji wa muji wowote au watu wa jamaa yoyote wakigombana wao kwa wao, muji ule au jamaa ile haitadumu. Na kama Shetani akimufukuza Shetani anajigombanisha yeye mwenyewe, nao ufalme wake utaanguka. Ninyi munasema kwamba ninafukuza pepo kwa uwezo wa Belzebuli. Basi watu wa kikundi chenu wanawafukuza kwa uwezo wa nani? Watu hao wanashuhudia kwa njia ya matendo yao kwamba ninyi ni wakosaji! Kwa ngambo yangu ninafukuza pepo kwa uwezo wa Roho wa Mungu. Hii inaonyesha kwamba Ufalme wa Mungu umekwisha kufika kati yenu. “Hakuna mutu anayeweza kuingia ndani ya nyumba ya mwenye nguvu na kunyanganya vitu vyake, isipokuwa kwanza anamufunga. Na kisha anaweza kunyanganya vitu vyake vyote. “Asiyekuwa wa upande wangu ni adui yangu; na asiyekusanya pamoja nami, anasambaza. Kwa hiyo ninawaambia: watu wataweza kusamehewa zambi zote wanazofanya na matusi yao yote. Lakini mutu anayetukana Roho Mutakatifu hatasamehewa. Kila mutu anayesema vibaya juu ya Mwana wa Mutu atasamehewa, lakini kila mutu anayesema vibaya juu ya Roho Mutakatifu, hatasamehewa katika ulimwengu huu, wala katika ule unaokuja. “Muti ukiwa muzuri, matunda yake yatakuwa mazuri vilevile; nao muti ukiwa mubaya, matunda yake yatakuwa mabaya vilevile. Kwa maana muti unatambulikana kwa matunda yake. Ninyi kikundi cha nyoka! Namna gani ninyi munaokuwa wabaya, munaweza kusema maneno mazuri? Kwa maana kinywa kinasema maneno yanayojaa ndani ya moyo. Mutu muzuri anatwaa vitu vizuri toka ndani ya akiba yake nzuri, naye mutu mubaya anatwaa vitu vibaya toka ndani ya akiba yake mbaya. “Ninawaambia wazi kwamba kwa Siku ya hukumu, watu watasamba kila neno lisilokuwa na maana walilosema. Kwa maana kila mutu atapata sheria au kupata azabu kufuatana na maneno yake.” Halafu walimu wamoja wa Sheria na Wafarisayo wamoja wakamwambia Yesu: “Mwalimu, tunataka kuona kitambulisho toka kwako.” Yesu akawajibu: “Watu wa kizazi kibaya na kinachokosa uaminifu mbele ya Mungu, wanataka kuona kitambulisho. Lakini hawataona kitambulisho isipokuwa kitambulisho cha nabii Yona. Kwa maana, kama vile Yona alivyobaki ndani ya tumbo la samaki mukubwa kwa muda wa siku tatu, muchana na usiku, ndivyo vilevile Mwana wa Mutu atakavyobaki ndani ya udongo kwa muda wa siku tatu, muchana na usiku. Kwa Siku ya hukumu, watu wa Ninawe watasimama nanyi watu wa kizazi hiki na kuwashitaki, kwa sababu wao waligeuka toka zambi zao waliposikia mahubiri ya Yona. Hapa kuna yule anayekuwa mukubwa kupita Yona! Vilevile kwa Siku ya hukumu malkia toka kusini atasimama na watu wa kizazi hiki na kuwashitaki, kwa sababu yeye alitoka mbali sana kuja kusikia maneno ya hekima ya mufalme Solomono. Hapa kuna yule anayekuwa mukubwa kumupita Solomono! “Wakati pepo imekwisha kutoka ndani ya mutu, inazungukazunguka katika jangwa kutafuta nafasi ya kupumzikia. Naye asipopata nafasi ile, anasema: ‘Nitarudi ndani ya nyumba yangu nilimotoka.’ Anaporudi, anaikuta wazi bila kitu, nayo imefagiliwa na kupambwa vizuri. Halafu anakwenda kutwaa pepo wengine saba wanaokuwa wabaya kumupita, nao wote wanakuja kuingia na kukaa mule. Na hali ya mwisho ya mutu yule inageuka mbaya kuliko hali yake ya kwanza. Na hivi ndivyo itakavyokuwa kwa watu wa kizazi hiki kibaya.” Yesu alipokuwa hajamaliza kusema na lile kundi la watu, mama yake na wandugu zake wakafika. Walisimama inje wakitaka kusemezana naye. Halafu mutu mumoja akamwambia: “Angalia, mama yako na wandugu zako wako inje; wanataka kusemezana nawe.” Yesu akamujibu mutu yule: “Ni nani ndiye mama yangu, na nani ndio wandugu zangu?” Kisha akawanyooshea wanafunzi wake mukono, na kusema: “Angalia, hawa ndio mama yangu na wandugu zangu. Kwa maana yeyote anayefanya mapenzi ya Baba yangu anayekuwa katika mbingu, huyu ndiye ndugu yangu, dada yangu na mama yangu.” Siku ile ile, Yesu akatoka ndani ya nyumba na kwenda kuikaa pembeni ya ziwa kwa kufundisha. Na kuona kundi kubwa la watu waliokusanyika karibu naye, akapanda ndani ya chombo na kukaa humo, nao watu walibaki wakisimama inchi kavu. Halafu akawafundisha mambo mengi akitumia mifano, akasema: “Mutu mumoja alikwenda kupanda mbegu. Alipokuwa akipanda mbegu katika shamba lake, zimoja zikaanguka pembeni ya njia, nao ndege wakakuja na kuzikula. Zingine zikaanguka pahali penye mawe, pasipokuwa udongo mwingi. Nazo zikaota upesi, kwa sababu hapakukuwa udongo mwingi. Wakati jua lilipokuwa kali, likazichoma, na kwa sababu hazikukuwa na mizizi mikubwa, zikakauka. Mbegu zingine zikaanguka katikati ya miiba. Ile miiba ikaota na kuzisonga. Lakini mbegu zingine zikaanguka katika udongo muzuri na kutoa matunda: zimoja zikazaa punje mia moja, zingine makumi sita na zingine makumi tatu. Basi mwenye kuwa na masikio ya kusikia, asikie!” Wanafunzi wa Yesu wakamwendea na kumwuliza: “Kwa sababu gani unasema na watu hawa ukitumia mifano?” Akawajibu: “Ninyi mumefunuliwa kujua siri ya Ufalme wa mbinguni, lakini kwao si vile. Kwa maana mutu anayekuwa na kitu ataongezewa kingine, naye atakuwa na vitu vingi. Lakini mutu asiyekuwa na kitu, ataondolewa hata kile kidogo anachokuwa nacho. Ni kwa sababu hiyo ninasema nao kwa kutumia mifano: kwa kuwa wanaangalia, lakini hawaoni, nao wanasikiliza lakini hawasikii wala hawafahamu. Hivi yametimia kwao maneno haya yaliyosemwa na Mungu kwa njia ya nabii Isaya: ‘kusikia, mutasikia, lakini hamutafahamu; kuangalia, mutaangalia, lakini hamutaona. Maana mioyo ya watu hawa imegeuka migumu, wameziba masikio yao, nao wamefunga macho yao, kusudi wasipate kuona, nao wasipate kusikia, wala wasipate kunigeukia, nami ningewaponyesha.’ “Lakini heri kwenu, kwa sababu macho yenu yanaona na masikio yenu yanasikia! Kweli ninawaambia: manabii wengi na wenye haki wengi walitamani kuona mambo munayoona, lakini hawakuyaona, na kusikia maneno munayosikia, lakini hawakuyasikia. “Basi musikilize maana ya ule mufano wa mupandaji wa mbegu. Pahali zile mbegu zilipoanguka pembeni ya njia, ni mufano wa watu wanaosikia habari ya Ufalme na kukosa kuielewa. Na kisha yule mwovu Shetani anakuja na kuondoa mbegu zilizopandwa ndani ya mioyo yao. Udongo wenye mawe pahali mbegu zilipoanguka ni mufano wa watu wanaosikia Neno la Mungu, na mara moja wanalipokea kwa furaha. Lakini halizami ndani yao kama mizizi. Wanalishika kwa muda mufupi tu. Wakati taabu na mateso vinapowafikia kwa ajili ya Neno la Mungu, mara moja, wanaanguka. Pahali zile mbegu zilipoanguka katika miiba, ni mufano wa wale wanaosikia Neno la Mungu, lakini masumbuko ya dunia hii na udanganyifu wa mali vinasonga lile neno linalokuwa ndani yao na kulizuiza kuzaa matunda. Pahali zile mbegu zilipoanguka katika udongo muzuri ni mufano wa watu wanaosikia Neno la Mungu na kulielewa. Nao wanazaa matunda; wamoja matunda mia moja, wengine makumi sita na wengine makumi tatu.” Yesu akawaambia mufano mwingine, akisema: “Ufalme wa mbinguni unafanana na mutu mumoja aliyepanda mbegu nzuri ya ngano katika shamba lake. Lakini siku moja usiku, wote walipokuwa wakilala usingizi, adui wa mutu yule akakuja na kupanda nyasi katikati ya ngano; kisha akajiendea. Ngano ilipoota na kutoa masuke, nyasi zikaonekana vilevile. Watumishi wa mwenye shamba wakamwendea na kumwuliza: ‘Ee Bwana, si ulipanda mbegu nzuri katika shamba lako? Basi nyasi hizi zimetoka wapi?’ Naye akawajibu: ‘Ni adui aliyefanya vile.’ Basi watumishi wakamwuliza: ‘Unataka tuende kuongoa zile nyasi?’ Lakini akajibu: ‘Hapana, mukiongoa nyasi, labda mutafikia kuongoa ngano pamoja nazo. Muviache vyote viwili vikomae pamoja mpaka wakati wa mavuno. Wakati ule nitawaambia wavunaji: muongoe kwanza nyasi, nanyi muzilundike kwa mafungu mafungu kwa kuzichoma, na kisha mukusanye ngano na kuweka mavuno ndani ya gala yangu.’ ” Yesu akawaambia mufano mwingine akisema: “Ufalme wa mbinguni unafanana na mbegu ya haradali mutu mumoja aliyoitwaa na kuipanda katika shamba lake. Mbegu hii ni ndogo sana kuliko mbegu zote, lakini inapokwisha kuota, inakuwa kubwa zaidi kuliko mimea yote, hata ndege wanakuja na kujenga chicha zao katikati ya matawi yake.” Yesu akawaambia tena mufano mwingine, akisema: “Ufalme wa mbinguni unafanana na chachu mwanamuke mumoja aliyoitwaa na kuichanga na vipimo vitatu vya unga kwa kuponda mikate hata yote ikapata kuvimba.” Yesu aliwaambia makundi ya watu maneno hayo yote akitumia mifano. Yeye hakusema nao pasipo kutumia mifano. Ilitokea vile kusudi yatimie maneno yaliyosemwa kwa njia ya nabii: “Nitasema nao kwa mifano, nitawaambia maneno yaliyofichwa tangu kuumbwa kwa dunia.” Halafu Yesu akaagana na makundi ya watu na kurudi kwenye nyumba. Wanafunzi wake wakamwendea na kumwambia: “Utufasirie maana ya ule mufano wa nyasi katika shamba.” Naye akawajibu: “Yule anayepanda mbegu nzuri ni Mwana wa Mutu. Shamba ni dunia. Mbegu nzuri ni washiriki wa Ufalme. Nyasi ni washiriki wa yule Mwovu Shetani. Adui aliyepanda nyasi ni Shetani. Mavuno ni mwisho wa dunia, nao wavunaji ni wamalaika. Kama vile nyasi zinavyoongolewa kwa kuchomwa katika moto, ndivyo itakavyokuwa vilevile kwa mwisho wa dunia. Mwana wa Mutu atawatuma wamalaika wake, nao watakusanya toka katika Ufalme wake watu wote wanaowaangusha wengine katika zambi pamoja na wote wanaofanya maovu. Nao watawatupa ndani ya furu la moto, na mule watalia na kusaga meno. Lakini wenye haki watametameta kama jua katika Ufalme wa Baba yao. Mwenye kuwa na masikio ya kusikia, asikie!” “Ufalme wa mbinguni unafanana na mali iliyofichwa katika shamba moja. Mutu mumoja alipoiona, akaificha tena. Halafu kwa furaha kubwa akaenda kuuzisha vitu vyake vyote na kununua lile shamba. “Ufalme wa mbinguni unafanana vilevile na muchuuzi mumoja aliyetafuta kununua ushanga muzuri. Alipoona ushanga mumoja muzuri sana, akaenda kuuzisha vitu vyake vyote na kuununua. “Ufalme wa mbinguni unafanana vilevile na wavuvi wamoja waliotupa wavu ndani ya ziwa, nao ukakusanya samaki wa kila namna. Wakati wavu ulipojaa, wavuvi wakaukokota inchi kavu. Halafu wakaikaa kwa kuchagua samaki: wakaweka samaki wazuri ndani ya vyombo na kutupa samaki wabaya. Ni hivi itakavyokuwa kwa mwisho wa dunia. Wamalaika watakuja na kuwatenga watu wabaya na watu wazuri. Na halafu watawatupa watu wabaya ndani ya furu la moto; na mule watalia na kusaga meno.” Yesu akawauliza watu: “Mumeelewa maneno hayo yote?” Nao wakamujibu: “Ndiyo.” Kisha akawaambia: “Basi, kila mwalimu wa Sheria aliyefundishwa katika Ufalme wa mbinguni, anafanana na mwenye nyumba anayetwaa vitu vipya na vitu vya zamani pamoja toka katika akiba yake.” Yesu alipomaliza kusema mifano hiyo, akaondoka kule na kwenda katika muji wake mwenyewe. Kule akaanza kuwafundisha watu katika nyumba zao za kuabudia, nao walishangaa na kuuliza: “Huyu amepata hekima na miujiza hii kutoka wapi? Huyu si mwana wa yule seremala? Mama yake si Maria? Nao Yakobo, Yosefu, Simoni na Yuda si wandugu zake? Na wadada zake, si wanaishi hapa kati yetu? Basi amepata mambo haya yote kutoka wapi?” Na kwa hiyo akakuwa kikwazo kwao. Lakini Yesu akawaambia: “Nabii hakosewi heshima fasi zote, isipokuwa tu katika muji wake na katika jamaa yake.” Na hivi kwa sababu ya kutokuamini kwa watu hao, Yesu hakufanya miujiza mingi kule. Katika siku zile, Herode, liwali wa jimbo la Galilaya, akasikia habari za Yesu. Halafu akawaambia wasimamizi waliokuwa chini yake: “Mutu huyu ni Yoane Mubatizaji aliyefufuka! Ni kwa sababu hii amepata uwezo wa kufanya miujiza.” Herode alikuwa amemukamata Yoane akamufunga minyororo na kumutia ndani ya kifungo. Herode alifanya vile kwa sababu ya Herodia, muke wa ndugu yake Filipo. Naye Yoane alikuwa amemwambia Herode kwamba hana sheria ya kumwoa yule muke wa ndugu yake. Herode alitaka kumwua Yoane, lakini aliwaogopa watu kwa maana wote walimuhesabia Yoane kuwa nabii. Na ilikuwa kwa sikukuu ya kuzaliwa kwa Herode, binti ya Herodia akacheza mbele ya wote walioalikwa. Binti yule akamupendeza Herode sana hata akamwahidi kwa kiapo kwamba atamupa kitu chochote atakachomwomba. Na kwa ajili ya kusukumwa na mama yake, yule binti akamwambia Herode: “Unipe hapa hapa ndani ya sahani kichwa cha Yoane Mubatizaji!” Mutawala huyu akahuzunika, lakini kwa sababu ya viapo alivyotoa na kwa sababu ya waalikwa, akaamuru binti yule apewe kichwa kile. Basi akaamuru waende kukata kichwa cha Yoane ndani ya kifungo. Halafu wakaleta kile kichwa chake ndani ya sahani na kukitoa kwa yule binti, naye akakipeleka kwa mama yake. Wanafunzi wa Yoane wakakuja kubeba maiti yake na kuizika. Nao wakaenda kumwelezea Yesu habari ile. Yesu aliposikia habari hii, akaondoka pale ndani ya chombo, na kwenda peke yake kwa pahali penye ukiwa. Nayo makundi ya watu waliposikia vile, wakatoka katika miji yao na kumufuata Yesu kwa miguu. Yesu alipotoka ndani ya chombo, akaona kundi kubwa la watu, naye akawasikilia huruma, akawaponyesha wale waliokuwa wagonjwa kati yao. Na ilipokuwa magaribi, wanafunzi wake wakamufikia na kumwambia: “Hapa ni pori na sasa ni magaribi. Uage kundi hili kusudi waende katika vijiji kwa kujinunulia vyakula.” Lakini Yesu akawajibu: “Si lazima waende; ninyi wenyewe muwape chakula.” Lakini wao wakamujibu: “Hapa tuko tu na mikate mitano na samaki mbili.” Yesu akawaambia: “Muvilete hapa.” Kisha kuwaamuru watu waikae juu ya majani, Yesu akatwaa ile mikate mitano na samaki mbili, akainua macho mbinguni, akamushukuru Mungu. Akamega ile mikate, akawapa wanafunzi wake, nao wakaigawanya kwa kundi la watu. Watu wote wakakula na kushiba. Kisha wanafunzi wakaokota vipande vya mikate vilivyobaki, wakajaza vitunga kumi na viwili. Hesabu ya watu waliokula ilikuwa yapata wanaume elfu tano, pasipo kuhesabu wanawake na watoto. Mara moja kisha mambo hayo, Yesu akawalazimisha wanafunzi wake waingie ndani ya chombo na kumutangulia ngambo ingine ya ziwa. Kwa wakati ule yeye alibaki akiaga lile kundi la watu. Kisha kuagana nao, akapanda kwenye kilima peke yake kwa kuomba. Na giza lilipoingia, alikuwa angali kule peke yake, lakini chombo kilikuwa kimekwisha kufika mbali sana na inchi kavu, kikirushwarushwa na zoruba, kwa maana upepo ulikuwa ukitokea mbele. Ilipokuwa karibu na mapambazuko, Yesu akawafikia wanafunzi wake, akitembea juu ya maji. Nao walipomwona akitembea juu ya maji wakashikwa na hofu, wakisema: “Ni muzimu!” Nao wakaanza kulalamika kwa ajili ya woga. Lakini mara moja Yesu akasema nao, akiwaambia: “Mujipe moyo, ni mimi! Musiogope!” Basi Petro akamwambia: “Bwana, ikiwa kweli ni wewe, utoe amri kusudi nifike pale unapokuwa, nikitembea juu ya maji.” Naye Yesu akamujibu: “Kuja.” Halafu Petro akatoka ndani ya chombo, akaanza kutembea juu ya maji kumufikia Yesu. Lakini alipoona upepo, akaogopa, na kwa vile alivyoanza kuzama ndani ya maji, akalalamika akisema: “Bwana, uniokoe!” Mara moja Yesu akanyoosha mukono, akamushika na kumwambia: “Ee wewe mwenye imani ndogo! Kwa sababu gani uliona shaka?” Nao wote wawili walipopanda ndani ya chombo, upepo ukatulizana. Basi wanafunzi waliokuwa ndani ya chombo wakapiga magoti mbele ya Yesu, wakisema: “Kweli wewe ni Mwana wa Mungu!” Walipokwisha kuvuka ziwa, wakafika pande za Genezareti. Na watu wa kule walipomutambua Yesu, wakatuma habari katika sehemu zile zote. Halafu wakamuletea wagonjwa wote na kumusihi awaruhusu waguse hata upindo wa nguo yake tu. Nao wote waliougusa walipona. Wafarisayo na walimu wa Sheria wakamufikia Yesu kutoka Yerusalema. Basi wakamwuliza: “Kwa sababu gani wanafunzi wako wanavunja desturi za babu zetu kwa kula chakula pasipo kunawa mikono?” Yesu akawajibu: “Na ninyi, kwa sababu gani munavunja amri ya Mungu kwa kufuata desturi zenu? Kwa maana Mungu alisema: ‘Uwaheshimu baba yako na mama yako.’ Naye alisema vilevile: ‘Anayelaani baba yake au mama yake anapaswa kuuawa.’ Lakini ninyi munasema kwamba mutu akiwa na kitu ambacho angeweza kuwasaidia baba yake au mama yake, lakini akimwambia kwamba amekitoa sadaka kwa Mungu, basi, hapaswi tena kumusaidia baba yake. Hivi munazarau Neno la Mungu kwa kufuata desturi zenu. Ninyi wanafiki! Isaya alitabiri vema juu yenu, wakati aliposema maneno haya: ‘Watu hawa wananiheshimu kwa midomo yao. Lakini mioyo yao ni mbali nami. Ibada wanayonifanyia ni ya bure, sababu mafundisho yao yanalingana na kanuni za watu tu.’ ” Kisha Yesu akaita kundi la watu na kuwaambia: “Musikilize na kuelewa maneno nitakayowaambia. Kitu kinachoingia ndani ya kinywa cha mutu hakiwezi kumuchafua. Lakini ni kile kinachotoka ndani ya kinywa chake ndicho kinachomuchafua.” Halafu wanafunzi wakamufikia na kumwuliza: “Unajua kwamba Wafarisayo walikwazwa kwa kusikia maneno hayo uliyosema?” Yesu akajibu: “Wao ni kama mumea usiopandwa na Baba yangu wa mbinguni, utakaopaswa kuongolewa. Muwaache! Wao ni vipofu, wanaongoza vipofu wengine. Na kama kipofu akimwongoza kipofu mwenzake, wote wawili wanatumbukia ndani ya shimo.” Halafu Petro akamwambia: “Utuelezee maana ya mufano huu.” Yesu akamujibu: “Hata ninyi vilevile hamuwezi kuelewa? Hamwelewi kwamba kila kitu kinachoingia ndani ya kinywa, kinapita ndani ya tumbo na kisha kinatoka na kwenda katika choo? Lakini vyote vinavyotoka ndani ya kinywa ni vyenye kutoka kwanza ndani ya moyo wake, navyo vinamuchafua mutu. Kwa maana ndani ya moyo munatoka mawazo mabaya yanayoleta uuaji, uzinzi, uasherati, wizi, ushuhuda wa uongo na matukano. Mambo haya ndiyo yanayomuchafua mutu! Lakini kula pasipo kunawa mikono hakuwezi kumuchafua mutu.” Yesu akaondoka pale na kwenda pande za karibu na muji wa Tiro na wa Sidona. Mwanamuke mumoja Mukanana aliyeishi katika pande zile akamufikia, akilalamika, akisema: “Ee Bwana, mwana wa Daudi, unihurumie! Binti yangu anateswa sana na pepo.” Lakini Yesu hakumujibu hata neno moja. Halafu wanafunzi wake wakamufikia na kumusihi: “Umwambie aende kwa maana anatuuzi na makelele.” Naye Yesu akajibu: “Nimetumwa tu kwa taifa la Waisraeli, wanaokuwa kama kondoo wanaopotea.” Lakini mwanamuke yule akapiga magoti mbele yake na kumwambia: “Ee Bwana, unisaidie!” Yesu akamujibu: “Si vizuri kukamata chakula cha watoto na kukitupia imbwa.” Yule mwanamuke akasema: “Ndiyo, Bwana, unasema ukweli, lakini hata imbwa wanazoea kula makombo yanayoanguka chini ya meza ya wabwana wao.” Halafu Yesu akamujibu: “Wewe mwanamuke, imani yako ni kubwa! Ifanyike kwako sawa ulivyoomba.” Na binti yake akapona tangia saa ile ile. Yesu akaondoka kule, akapita pembeni ya ziwa la Galilaya. Kisha akapanda kwenye kilima, naye akaikaa pale. Halafu makundi mengi ya watu wakamufikia, wakimuletea vilema, vipofu, viwete na wabubu. Wakawaweka mbele ya Yesu, naye akawaponyesha. Yale makundi ya watu wakashangaa sana wakati walipowaona wabubu wanasema, vilema wanakuwa wazima, viwete wanatembea, na vipofu wanaona. Nao wakamusifu Mungu wa Waisraeli. Yesu akawaita wanafunzi wake, na kuwaambia: “Ninawasikilia watu hawa huruma, kwa sababu wamekaa nami sasa kwa muda wa siku tatu, nao hawana chakula tena. Nami sitaki kuagana nao pasipo kula, kusudi wasiregee katika njia.” Nao wanafunzi wake wakamujibu: “Hapa katika pori, tutaweza kupata wapi chakula cha kushibisha kundi kubwa kama hili?” Yesu akawauliza: “Muko na mikate ngapi?” Nao wakajibu: “Tuko na mikate saba na samaki ndogo chache.” Basi Yesu akawaamuru watu waikae chini. Kisha akatwaa ile mikate saba na zile samaki, akamushukuru Mungu, akaimega na kuwapa wanafunzi wake wavigawanye kwa watu. Wote wakakula na wakashiba. Kisha wanafunzi wakaokota vipande vilivyobaki, wakajaza vitunga saba. Watu waliokula walikuwa wanaume elfu ine, pasipo kuhesabu wanawake na watoto. Kisha kuaga yale makundi ya watu, Yesu akaingia ndani ya chombo, na kwenda pande za Magadani. Wafarisayo na Wasadukayo wakamufikia Yesu. Nao wakamupima wakimwomba awaonyeshe kitambulisho kinachohakikisha kwamba uwezo wake unatoka kwa Mungu. Lakini akawajibu: “Kwa wakati wa magaribi munapoona kwamba mawingu ni meupe, munasema kwamba hali ya hewa itakuwa nzuri kesho yake. Na asubui munapoona kwamba mawingu ni meusi munasema kwamba mvua itanyesha. Munajua kutambua hali ya mawingu, lakini hamuwezi kujua vitambulisho vya nyakati hizi. Watu wa kizazi kibaya na kinachokosa uaminifu mbele ya Mungu wanataka kuona kitambulisho. Lakini hawataonyeshwa kitambulisho isipokuwa kitambulisho cha nabii Yona.” Kisha Yesu akawaacha na kujiendea. Wakati wanafunzi walipovuka ziwa kwenda ngambo ingine, walikuwa wamesahau kupeleka mikate. Yesu akawaambia: “Muangalie vizuri, mujiepushe na chachu ya Wafarisayo na Wasadukayo.” Wanafunzi wakaanza kusemezana hivi wao kwa wao: “Anasema hivi kwa sababu hatuna mikate.” Yesu akatambua maneno waliyosema, basi akawauliza: “Ee ninyi wenye imani ndogo, sababu gani munasemezana kati yenu juu ya kukosa mikate? Hamujaelewa bado? Hamukumbuki ile mikate mitano niliyoshibisha nayo watu elfu tano, nayo ile hesabu ya vitunga mulivyojaza? Hamukumbuki vilevile ile mikate saba niliyoshibisha nayo watu elfu ine, na ile hesabu ya vitunga mulivyojaza? Namna gani hamwelewi kwamba sisemi nanyi juu ya mikate, nilipowaambia kwamba mujiepushe na chachu ya Wafarisayo na Wasadukayo.” Halafu wanafunzi wakafahamu kwamba Yesu hakuwaambia kwamba wafanye angalisho na chachu ya mikate, lakini na mafundisho ya Wafarisayo na Wasadukayo. Yesu alipofika pande za muji Kaisaria Filipi, akawauliza wanafunzi wake: “Watu wanasema kwamba Mwana wa Mutu ni nani?” Nao wakamujibu: “Wamoja wanasema kwamba yeye ni Yoane Mubatizaji; wengine wanasema kwamba yeye ni Elia, na wengine wanasema ni Yeremia au mumoja wa manabii wengine.” Halafu Yesu akawauliza: “Na ninyi munasema kwamba mimi ni nani?” Simoni Petro akamujibu: “Wewe ni Kristo, Mwana wa Mungu Mwenye Uzima.” Halafu Yesu akamwambia: “Heri kwako, wewe Simoni mwana wa Yona, kwa maana hakuna mutu aliyekufunulia neno hili isipokuwa Baba yangu anayekuwa mbinguni. Nami sasa ninakuambia: ewe Petro, wewe ni jiwe, na juu ya jiwe hili, nitajenga musingi wa kanisa langu, na hata uwezo wa lufu hautaweza kulishinda. Nitakupa funguo za Ufalme wa mbinguni; chochote utakachokikataza katika dunia, kitakatazwa mbinguni vilevile, na chochote utakachokiruhusu katika dunia, kitaruhusiwa mbinguni vilevile.” Kisha Yesu akawakataza sana wanafunzi wake wasimwambie mutu kwamba yeye ndiye Kristo. Tangia wakati ule Yesu akaanza kuwaambia wanafunzi wake waziwazi kwamba ni sherti kwake kwenda Yerusalema, ateswe kule na wasimamizi wa watu, wakubwa wa makuhani na walimu wa Sheria, auawe, na kwa siku ya tatu kisha kufa kwake, atafufuka. Basi Petro akamwita Yesu pembeni na kuanza kumukaripia, akisema: “Ee Bwana, isikuwe vile! Mambo yale hayatakufikia hata kidogo!” Lakini Yesu akageuka na kumwambia: “Ondoka hapa karibu nami, wewe Shetani! Wewe ni kikwazo kwangu, kwa maana mawazo yako si ya Mungu, lakini ni ya kimutu.” Kisha Yesu akawaambia wanafunzi wake: “Kama mutu akitaka kunifuata, ajikane yeye mwenyewe, lakini ajitolee kwa kubeba musalaba wake na kunifuata. Kwa maana mutu anayetaka kulinda uzima wake, ataupoteza; lakini yule atakayetoa uzima wake kwa ajili yangu, ataupata tena. Ni faida gani kwa mutu kupata utajiri wote wa dunia, lakini anapoteza uzima wake? Hakuna kitu mutu anachoweza kutoa kwa kukomboa uzima wake. Kwa maana Mwana wa Mutu atakuja na wamalaika akitukuzwa na Baba yake, halafu atamulipa kila mutu kufuatana na matendo yake. Kweli ninawaambia: wamoja kati ya watu wanaokuwa hapa hawatakufa mbele hawajamwona Mwana wa Mutu akikuja katika Ufalme wake.” Nyuma ya siku sita, Yesu aliwatwaa Petro, Yakobo na ndugu yake Yoane, na kuwapeleka kwenye mulima murefu. Nao walikuwa kule peke yao. Na kule sura ya Yesu ikageuka wazi mbele yao. Uso wake ukangaa kama jua, nazo nguo zake zikametameta kama mwangaza. Halafu Musa na Elia wakiwa wakisemezana na Yesu, wakawatokea wale wanafunzi. Basi Petro akamwambia Yesu: “Bwana, ni vizuri kuona kwamba sisi tuko hapa. Ukitaka, nitajenga hapa vibanda vitatu, kimoja chako, kimoja cha Musa na kingine cha Elia.” Naye alipokuwa angali akisema, wingu lenye kuangaza likawafunika, na sauti ikasikilika toka katikati ya lile wingu ikisema: “Huyu ni Mwana wangu mupendwa, ninapendezwa naye sana. Mumusikilize!” Wanafunzi wale waliposikia sauti ile, wakaogopa sana, wakaanguka uso mpaka chini. Lakini Yesu akawajongelea, akawagusa na kuwaambia: “Musimame, musiogope.” Nao walipoinua macho yao, hawakumwona mutu mwingine, isipokuwa Yesu peke yake. Walipokuwa wakishuka toka kwa mulima, Yesu akawaamuru: “Musimwelezee mutu mambo muliyoona mpaka Mwana wa Mutu atakapofufuka.” Kisha wanafunzi wakamwuliza: “Kwa nini basi walimu wa Sheria wanasema kwamba sherti Elia arudi kwanza?” Yesu akawajibu: “Hakika Elia anapaswa kurudi kwanza kutengeneza mambo yote. Lakini ninawaambia kama Elia amekwisha kurudi, nao hawakumutambua, lakini walimutendea yote waliyotaka. Ni vile ndivyo Mwana wa Mutu atateswa nao vilevile.” Halafu wanafunzi wakafahamu kwamba alisema nao juu ya Yoane Mubatizaji. Yesu na wanafunzi wake waliendelea hata wakafika kwenye kundi la watu. Pale mutu mumoja akamwendea Yesu, akapiga magoti mbele yake, na kusema: “Bwana, ninakuomba umusikilie mwana wangu huruma kwa maana anateswa sana na ugonjwa wa kifafa. Mara nyingi anaanguka katika moto na ndani ya maji. Nilimuleta kwa wanafunzi wako, lakini hawakuweza kumuponyesha.” Na Yesu akawaambia wanafunzi wake: “Ee ninyi watu wa kizazi kisichoamini Mungu na chenye kupotoka. Nitakaa pamoja nanyi tena mpaka wakati gani? Nitawavumilia tena mpaka wakati gani? Muniletee mutoto hapa.” Yesu akamukaripia yule pepo aliyekuwa ndani ya yule mutoto, naye akamwacha, na tangia saa ile ile yule mutoto akapona. Kisha wanafunzi wakamufikia Yesu, wakiwa peke yao, na kumwuliza: “Kwa nini sisi hatukuweza kumufukuza yule pepo?” Yesu akawajibu: “Kwa sababu imani yenu ni ndogo. Kweli ninawaambia kama mukiwa na imani, hata ikiwa tu kama punje ndogo sana ya mbegu ya haradali, mutaweza kuuambia mulima huu: ‘Toka hapa uende kule,’ nao utatoka pale. Hakuna kitu chochote kitakachokosa kuwezekana kwenu. [ Lakini pepo wa namna hii hawawezi kufukuzwa isipokuwa tu kwa njia ya maombi na kufunga kula chakula.]” Wanafunzi walipokuwa pamoja katika jimbo la Galilaya, Yesu akawaambia: “Mwana wa Mutu atatolewa katika mikono ya watu, nao watamwua, lakini kwa siku ya tatu kisha kufa kwake, atafufuka.” Halafu wanafunzi wakahuzunika sana. Yesu na wanafunzi wake walipofika katika muji Kapernaumu, walipishaji wa kodi ya hekalu wakamwendea Petro na kumwuliza: “Si mwalimu wenu analipa kodi ya hekalu?” Petro akawajibu: “Ndiyo, analipa.” Petro alipoingia ndani ya nyumba, mbele hajasema kitu Yesu akamwuliza: “Simoni, unafikiri nini? Wafalme wa dunia wanawalipisha watu gani kodi au malipo mengine mbalimbali? Ni watu wa jamaa zao wenyewe au watu wengine?” Petro akamujibu: “Watu wengine.” Na Yesu akamwambia: “Basi ni kusema kwamba watu wa jamaa zao wako na ruhusa ya kutolipa. Lakini haifai kuwakwaza. Kwa hiyo kwenda kwenye ziwa, na utupe ndoana ndani ya maji. Na samaki wa kwanza utakayemunasa, ufungue kinywa chake, nawe utaona kikoroti cha feza. Ukikamate na kukitoa kwa kulipa kodi kwa ajili yetu sisi wawili.” Wakati ule wanafunzi wakamufikia Yesu, wakamwuliza: “Ni nani anayekuwa mukubwa katika Ufalme wa mbinguni?” Halafu akamwita mutoto mudogo, akamusimamisha katikati yao na kusema: “Kweli ninawaambia: kama musipogeuka na kuwa sawasawa na mutoto mudogo, hamutaingia katika Ufalme wa mbinguni hata kidogo. Basi kila mutu atakayekuwa munyenyekevu kama huyu mutoto mudogo, ndiye atakayekuwa mukubwa katika Ufalme wa mbinguni. Naye anayemupokea mutoto mudogo kama huyu kwa ajili ya jina langu, ananipokea mimi. “Lakini anayeangusha mumoja wa hawa wadogo wanaoniamini, ingalikuwa heri afungiwe jiwe kubwa la kusagia katika shingo na kuzamishwa ndani ya bahari. Ole kwa dunia kwa ajili ya vikwazo vinavyokuwa ndani yake! Vikwazo haviwezi kosa kutokea, lakini ole kwa mutu yule anayevileta! “Kama mukono wako au muguu wako ukikukosesha, uukate na kuutupa mbali! Ni heri kwako kuingia kwenye uzima wa kweli ukikuwa na mukono mumoja au ukikuwa kilema. Hiyo ni vizuri kuliko kuwa na mikono miwili au miguu miwili na kutupwa katika moto kwa milele. Na kama jicho lako likikukosesha, uliongoe na kulitupa mbali! Ni heri kwako kuingia pahali utakapopata uzima wa kweli ukikuwa na jicho moja kuliko kuwa na macho mawili na kutupwa katika moto wa jehenamu. “Mufanye angalisho, musimuzarau mumoja wa hawa wadogo; kwa sababu ninawaambia kwamba wamalaika wao wanaokuwa mbinguni wako siku zote karibu na Baba yangu anayekuwa mbinguni. [ Kwa maana Mwana wa Mutu alikuja kuokoa yule aliyepotea.] “Munafikiri nini? Kama mutu akiwa na kondoo mia moja, na mumoja wao akipotea, hatawaacha wale wengine makumi tisa na tisa juu ya mulima na kwenda kumutafuta yule aliyepotea? Na kama akimupata yule kondoo, kweli ninawaambia, anamufurahia kuliko wale makumi tisa na tisa waliobaki bila kupotea. Ni hivi vilevile Baba yenu anayekuwa mbinguni hataki hata mumoja wa hawa wadogo kupotea. “Kama ndugu yako akikukosea, umwendee kwa kumwonyesha kosa lake, mukiwa ninyi wawili peke yenu. Na kama akikusikia, unarudiliana na ndugu yako. Lakini kama akikataa kukusikia, utwae mutu mumoja au wawili na kumwendea pamoja nao, kusudi kila neno lihakikishwe kwa ushuhuda wa watu wawili au watatu, sawa vile Maandiko Matakatifu yanavyosema. Na kama akikataa kuwasikia watu wale, upeleke habari kwa kanisa. Naye akikataa kusikia kanisa vilevile, umuhesabu kama mupagani na mutenda maovu sawa walipishaji wa kodi. “Hivi, kweli ninawaambia: chochote mutakachokikataza katika dunia kitakatazwa mbinguni vilevile, na chochote mutakachokiruhusu katika dunia, kitaruhusiwa mbinguni vilevile. “Kweli ninawaambia tena: wawili kati yenu hapa katika dunia wakipatana kwa kuomba juu ya kitu chochote, Baba yangu anayekuwa mbinguni atawapa kitu kile. Kwa maana pahali popote watu wawili au watatu wanapokusanyika kwa ajili ya jina langu, mimi ni pale katikati yao.” Kisha Petro akamwendea Yesu na kumwuliza: “Bwana, ndugu yangu akiendelea kunikosea, nitamusamehe mpaka mara ngapi? Mara saba inatosha?” Yesu akamujibu: “Hapana, sikuambii kwamba umusamehe mara saba tu, lakini mpaka mara makumi saba mara saba. Ni kwa sababu hii Ufalme wa mbinguni unafanana na mufalme mumoja aliyetaka kufanya hesabu ya madeni watumishi wake waliyokuwa nayo. Alipoanza kufanya hesabu ile, wakamuletea mutumishi mumoja aliyekuwa na deni lake la mamilioni ya feza. Na kwa kuona mutumishi yule hakukuwa na jinsi ya kulipa deni lile, bwana wake akaamuru auzishwe kuwa mutumwa, yeye na muke wake pamoja na watoto wake na vyote alivyokuwa navyo viuzishwe vilevile, kusudi apate kumulipa. Basi mutumishi yule akamupigia bwana wake magoti, akamusihi, akisema: ‘Ninakuomba univumilie, nami nitakulipa deni lako lote!’ Yule bwana akamusikilia mutumishi yule huruma, akamusamehe deni lile na kumwacha kwenda. “Mutumishi yule alipoondoka, akakutana na mumoja wa watumishi wenzake aliyekuwa na deni lake la vikoroti mia moja vya feza. Akamukamata na kumunyonganyonga shingo na kumulazimisha kulipa deni lake. Huyo mutumishi mwenzake akamupigia magoti na kumusihi, akisema: ‘Ninakuomba univumilie, nami nitakulipa deni lako!’ Lakini hakutaka, akamupeleka katika kifungo mpaka atakapolipa deni lile. Nao watumishi wenzake walipoona jambo hilo, wakahuzunika sana, wakaenda kumwelezea bwana wao yote yaliyotokea. Halafu yule bwana akamwita mutumishi yule na kumwambia: ‘Wewe ni mutumishi mubaya! Mimi nilikusamehe deni lako lote, kwa sababu ulinisihi. Wewe vilevile ulipaswa kumuhurumia mutumishi mwenzako sawa vile mimi nilivyokuhurumia.’ Basi yule bwana akakasirika sana, akamutoa mutumishi yule aazibiwe mpaka atakapolipa lile deni lake.” Yesu akaongeza kusema: “Ni hivi vilevile Baba yangu anayekuwa mbinguni atakavyowatendea ninyi, kama kila mumoja wenu asipomusamehe ndugu yake kwa moyo wake wote.” Yesu alipomaliza kusema maneno hayo akaondoka Galilaya. Akaenda katika jimbo la Yudea na kuvuka ngambo ya Yordani. Na makundi mengi ya watu wakamufuata, naye akawaponyesha wagonjwa kule. Wafarisayo wamoja wakamufikia kwa kumupima, wakamwuliza: “Sheria yetu inamuruhusu mutu kumufukuza muke wake haizuru kwa sababu gani?” Yesu akajibu: “Hamujasoma bado maneno yanayoandikwa katika Maandiko Matakatifu? ‘Kwa mwanzo Muumba aliumba mwanaume na mwanamuke,’ na kisha akasema: ‘Kwa sababu hii, mutu atawaacha baba yake na mama yake na kuungana na muke wake, nao wawili watakuwa mwili mumoja.’ Hivi wao si wawili tena, lakini wanakuwa mumoja. Basi mutu asitenganishe kile Mungu alichokiunganisha.” Halafu Wafarisayo wakamwuliza: “Kwa sababu gani basi Musa aliamuru kuandika barua ya kuachana wakati wa kumufukuza mwanamuke?” Yesu akawajibu: “Musa aliwapa ninyi ruhusa ya kuachana na wake wenu kwa sababu ya ugumu wa mioyo yenu. Lakini haikuamuriwa vile tangu mwanzo. Na sasa mimi ninawaambia: kila mutu anayeachana na muke wake, isipokuwa kwa sababu ya uzinzi tu, na kumwoa muke mwingine, anazini.” Wanafunzi wake wakamwambia: “Ikiwa hayo ndiyo mapaswa ya mume kwa muke, hakuna mafaa ya kuoa.” Yesu akawajibu: “Si watu wote wanaoweza kukubali neno hilo munalosema, isipokuwa tu wale wanaojaliwa na Mungu. Kulingana na hayo, watu wamoja hawawezi kuoa kwa sababu walizaliwa towashi, wengine wamefanywa kuwa towashi na watu, wengine wamejifanya vile wenyewe kwa sababu ya kutumikia Ufalme wa mbinguni. Anayeweza kukubali mafundisho haya, ayakubali!” Watu wamoja walimuletea Yesu watoto kusudi awawekee mikono na kuwaombea, lakini wanafunzi wakawakaripia watu wale. Lakini Yesu akawaambia wanafunzi wake: “Muwaache watoto wakuje kwangu, wala musiwakataze, kwa maana Ufalme wa mbinguni ni wa watu wanaokuwa sawasawa na wao.” Naye alipokwisha kuweka mikono juu yao, akaondoka pale. Kijana mumoja akamufikia Yesu na kumwuliza: “Mwalimu, nifanye jambo gani jema kusudi nipate uzima wa milele?” Yesu akamujibu: “Sababu gani unaniuliza juu ya jambo linalokuwa jema? Kuna mumoja tu anayekuwa mwema. Kama ukitaka kuingia pahali utakapopata uzima wa kweli, utii amri za Mungu.” Naye akauliza: “Amri gani?” Yesu akamujibu: “Usiue, usizini, usiibe, usishuhudie uongo, uwaheshimu baba yako na mama yako na kumupenda mwenzako sawa wewe mwenyewe.” Yule kijana akamwambia: “Nimetii hizo amri zote. Ninakosewa na nini tena?” Yesu akamujibu: “Ukitaka kuwa mutimilifu, kwenda uuzishe vitu unavyokuwa navyo, na uwape wamasikini mali zile, nawe utakuwa na akiba mbinguni. Kisha urudi, unifuate.” Lakini yule kijana aliposikia maneno hayo, akajiendea akihuzunika, kwa sababu alikuwa tajiri sana. Halafu Yesu akawaambia wanafunzi wake: “Kweli ninawaambia: ni vigumu sana kwa tajiri kuingia katika Ufalme wa mbinguni. Ninawaambia tena: ni kwepesi zaidi kwa ngamia kupita katika tundu la sindano, kuliko tajiri kuingia katika Ufalme wa Mungu.” Wanafunzi waliposikia maneno haya, wakashangaa sana na kuuliza: “Ni nani basi anayeweza kuokolewa?” Yesu akawaangalia na kuwaambia: “Jambo hilo haliwezi kutendeka kwa uwezo wa mwanadamu, lakini kwa uwezo wa Mungu, yote yanawezekana.” Halafu Petro akamwuliza: “Angalia, sisi tumeacha vyote na kukufuata wewe! Basi na sisi tutapata nini?” Yesu akawajibu: “Kweli ninawaambia: Katika ulimwengu mupya, Mwana wa Mutu atakapoikaa juu ya kiti chake cha kifalme chenye utukufu, ninyi kumi na wawili mulionifuata mutaikaa vilevile juu ya viti kumi na viwili vya kifalme kwa kuhukumu makabila kumi na mawili ya Waisraeli. Na kila mutu aliyeacha nyumba yake, kaka, dada, baba, mama, watoto au mashamba kwa ajili yangu, atapokea mara nyingi zaidi na kupewa uzima wa milele. Lakini wengi wanaokuwa wa kwanza watakuwa wa mwisho, na wengi wanaokuwa wa mwisho watakuwa wa kwanza. “Ufalme wa mbinguni unafanana na mutu mumoja mwenye shamba la mizabibu aliyetoka asubui mapema kwa kutafuta watu wa kutumika katika shamba lake. Akapatana na watumishi wamoja kuwalipa kila mutu kikoroti kimoja cha feza sawa na kawaida, naye akawatuma katika shamba lake. Ilipokuwa saa tatu za asubui, akatoka tena akawaona watu wengine wakisimama bure kwenye nafasi ya makutano. Akawaambia: ‘Ninyi vilevile muende kutumika katika shamba langu la mizabibu, nami nitawalipa sawa na haki yenu.’ Basi wakaenda. Mwenye shamba akatoka tena na saa sita, kisha na saa tisa, akafanya sawasawa mbele. Karibu na saa kumi na moja akatoka tena, naye akakuta watu wengine wakisimama pale kwenye nafasi ile. Akawauliza: ‘Sababu gani munasimama bure hapa muchana kutwa?’ Nao wakamujibu: ‘Kwa sababu hakuna mutu aliyetupatia kazi.’ Halafu akawaambia: ‘Ninyi vilevile muende kutumika katika shamba langu la mizabibu.’ “Ilipokuwa magaribi, mwenye shamba akamwambia musimamizi wake: ‘Uwaite watumishi na uwalipe mushahara wao, ukianzia kwa wale wa mwisho mpaka kwa wale wa kwanza.’ Wale walioanza kazi na saa kumi na moja ya magaribi wakakuja, na kila mutu akapokea kikoroti kimoja cha feza. Na wale waliotangulia kuanza kazi wakakuja, wakizani kwamba watapewa zaidi. Lakini nao vilevile wakapokea kila mutu kikoroti kimoja cha feza. Watu wale walipopokea mushahara ule, wakamunungunikia mwenye shamba. Wakasema: ‘Watumishi hawa wa mwisho wametumika kazi kwa saa moja tu, nawe umewalipa sawasawa na sisi tuliovumilia muchoko na jua kali kwa muchana kutwa!’ Lakini mwenye shamba akamujibu mumoja wao: ‘Rafiki, sikupunji kitu. Hatukupatana kwamba nitakulipa kikoroti kimoja cha feza kwa siku? Basi kamata mushahara wako na uende. Ilinipendeza mimi peke kumupa mutu wa mwisho mushahara unaolingana na wako. Sina haki ya kutumia mali yangu sawa ninavyotaka? Unapatwa na wivu kwa sababu mimi ni mwema?’ ” Yesu akaongeza kusema: “Ni hivi inavyokuwa vilevile: wanaokuwa wa mwisho watakuwa wa kwanza, nao wanaokuwa wa kwanza watakuwa wa mwisho.” Yesu alipokuwa katika njia kwenda Yerusalema, akaita wanafunzi wake kumi na wawili pembeni, akawaambia: “Angalia, tunapanda kwenda Yerusalema na kule Mwana wa Mutu atatolewa kwa wakubwa wa makuhani na kwa walimu wa Sheria. Nao watamuhukumu auawe na kumutoa katika mikono ya watu wa mataifa mengine. Nao watamuchekelea, watamupiga fimbo na kumutundika juu ya musalaba. Lakini kwa siku ya tatu kisha kufa kwake, atafufuka.” Wana wa Zebedayo pamoja na mama yao wakamufikia Yesu. Yule mama akapiga magoti mbele yake, kwa kumwomba kitu kimoja. Yesu akamwuliza: “Unataka nini?” Naye akamujibu: “Utakapokuwa katika Ufalme wako, uwaruhusu hawa wana wangu wawili kuikaa, mumoja kwa upande wako wa kuume na mwingine kwa upande wako wa kushoto.” Yesu akawaambia: “Hamujui kitu munachoomba. Munaweza kubeba muzigo wa mateso nitakaoubeba?” Nao wakamujibu: “Tunaweza.” Na Yesu akawaambia: “Hakika mutaubeba muzigo nitakaoubeba. Lakini kuikalisha mutu kwa upande wangu wa kuume au wa kushoto si kazi yangu. Ni Mungu peke yake atakayeweka watu aliowatayarisha kwenye nafasi zile.” Wanafunzi wengine kumi waliposikia maneno yale, wakachukizwa na wale wandugu wawili. Halafu Yesu akawaita wote pamoja na kuwaambia: “Munajua kwamba watawala wa mataifa wanayatawala kwa kinguvu, na wakubwa wao wanayagandamiza. Lakini isikuwe hivi katikati yenu. Anayetaka kuwa mukubwa kati yenu, sherti akuwe mutumishi wenu. Naye anayetaka kuwa wa kwanza, sherti akuwe mutumwa wenu. Kwa maana Mwana wa Mutu hakukuja kutumikiwa, lakini kutumikiana na kutoa maisha yake kusudi awakomboe watu wengi.” Yesu na wanafunzi wake walipokuwa wakitoka Yeriko, kundi kubwa la watu wakamufuata. Na kulikuwa vipofu wawili waliokuwa wakiikaa pembeni ya njia, nao wakasikia kwamba Yesu anapita. Kwa hiyo wakalalamika, wakisema: “Bwana, mwana wa Daudi, utusikilie huruma!” Kundi la watu wakawakaripia na kuwaambia wanyamaze. Lakini wale vipofu wakaendelea kulalamika kwa nguvu, wakisema: “Mwana wa Daudi, utusikilie huruma!” Yesu akasimama na kuwaita. Akawauliza: “Munataka niwafanyie nini?” Nao wakamujibu: “Bwana, tunakuomba utuponyeshe macho.” Yesu akawasikilia huruma. Akagusa macho yao, na mara moja wakapata kuona, nao wakamufuata. Yesu na wanafunzi wake wakakaribia kufika Yerusalema upande wa kijiji cha Betefage, karibu na mulima wa Mizeituni. Yesu akawatuma wawili kati ya wanafunzi wake, akawaambia: “Mwende katika kijiji kinachokuwa mbele yenu. Wakati mutakapofika kule, mara moja mutaona punda amefungwa na mwana-punda akiwa pamoja naye. Muwafungue na kuwaleta. Na kama mutu akiwauliza neno, mumwambie kama Bwana yuko na lazima ya kuwatumia. Na mara moja mutu yule atawaruhusu kuwapeleka.” Mambo hayo yote yalitokea, kusudi yatimie maneno yaliyosemwa kwa njia ya nabii: “Muwaambie wakaaji wa muji Sayuni: ‘Angalia, mufalme wenu anakuja kwenu. Yeye ni munyenyekevu, amepanda juu ya punda, juu ya mwana-punda, kitoto cha punda.’ ” Basi wale wanafunzi wakaenda, nao wakafanya sawa Yesu alivyowaagiza. Wakaleta punda pamoja na mwana-punda, wakatandika nguo juu yao na Yesu akaikaa juu ya nguo zile. Watu wengi wakatandika nguo zao katika njia, na wengine wakakata matawi ya miti na kuyatandika katika njia vilevile. Nalo kundi la watu waliomutangulia Yesu na lile la watu waliofuata nyuma yake, wakaanza kulalamika, wakisema: “Usifiwe wewe Mwana wa Daudi! Abarikiwe huyu anayekuja kwa jina la Bwana! Mungu asifiwe juu mbinguni!” Yesu alipoingia Yerusalema, muji wote ukavuma. Watu wakaulizana: “Huyu ni nani?” Kundi la watu wakajibu: “Huyu ni nabii Yesu wa Nazareti katika Galilaya.” Yesu akaingia ndani ya hekalu, naye akawafukuza watu wote waliokuwa wakiuzishia na kununulia vitu vyao ndani yake. Akapindua meza za wale waliobadilisha feza na viti vya wachuuzi wa njiwa. Akawaambia: “Imeandikwa hivi katika Maandiko Matakatifu: ‘Nyumba yangu itaitwa nyumba ya maombi.’ Lakini ninyi mumeigeuza kuwa nafasi ya makutano ya wanyanganyi!” Vipofu na viwete wakamufikia Yesu kule ndani ya hekalu, naye akawaponyesha. Lakini wakubwa wa makuhani na walimu wa Sheria wakachukizwa kwa kuona miujiza aliyoifanya na watoto waliokuwa wakilalamika katika hekalu, wakisema: “Usifiwe wewe, mwana wa Daudi!” Basi wakamwuliza Yesu: “Unasikia maneno watoto hawa wanayoyasema?” Yesu akawajibu: “Ndiyo. Lakini hamujasoma Maandiko Matakatifu yanayosema: ‘Kwa vinywa vya watoto wadogo hata wale wanaokuwa wachanga umetangaza sifa zako.’ ” Kisha akawaacha, akatoka inje ya muji wa Yerusalema, naye akaenda Betania na kulala kule. Kesho yake asubui, Yesu alipokuwa akirudia Yerusalema, akasikia njaa. Akaona muti wa tini pembeni ya njia, akaenda karibu nao, lakini hakuona kitu juu yake isipokuwa majani matupu. Halafu Yesu akaulaani muti ule akisema: “Wewe usitoe tena matunda tangu leo hata milele!” Na pale pale muti ule ukakauka. Wanafunzi walipoona jambo hilo, wakashangaa sana na kujiuliza: “Namna gani muti huu umekauka mara moja?” Yesu akawajibu: “Kweli ninawaambia: mukimwamini Mungu pasipo kuwa na shaka, hamutaweza kufanya tu kama nilivyotendea muti huu, lakini vilevile mutaweza kuuambia mulima huu: ‘Ondoka hapa, ujitupe katika bahari,’ na itakuwa vile. Na kitu chochote mutakachoomba, mukiamini, mutakipata.” Yesu akaingia ndani ya hekalu. Alipokuwa akifundisha, wakubwa wa makuhani pamoja na wasimamizi wa watu wakamufikia na kumwuliza: “Unafanya mambo haya kwa mamlaka gani? Ni nani aliyekupa mamlaka yale?” Yesu akawajibu: “Nitawauliza ulizo moja tu. Kama mukinijibu, mimi vilevile nitawaambia ni kwa mamlaka gani ninafanya mambo haya. Yoane alipata mamlaka ya kubatiza kutoka kwa nani? Kwa Mungu au kwa watu?” Nao wakaanza kupiga mafikiri pamoja na kusema: “Kama tukijibu kwamba mamlaka yake yalitoka kwa Mungu, atatuuliza: ‘Kwa sababu gani basi hamukumwamini?’ Lakini vilevile kwa kuwa tunaogopa watu hawa, hatuwezi kusema kwamba yalitoka kwa mutu; kwa maana watu hawa wote wanasadiki kwamba Yoane alikuwa nabii.” Basi wakamujibu Yesu: “Hatujui.” Naye akawaambia: “Nami vilevile sitawaambia ninyi ni kwa mamlaka gani ninafanya mambo haya.” Yesu akaongeza kusema: “Ninyi munafikiri nini juu ya habari hii? Kulikuwa mutu mumoja aliyekuwa na watoto wawili. Yeye akamwambia mutoto wa kwanza: ‘Mutoto wangu, ninataka uende leo kutumika katika shamba langu la mizabibu.’ Naye akamujibu: ‘Sitaki.’ Lakini kisha akageuza nia yake na kwenda kutumika. Halafu yule baba akamwambia mutoto wa pili sawa vile alivyomwambia yule wa kwanza. Naye akamujibu: ‘Ndiyo, baba,’ lakini hakwenda. Kati ya hawa wawili ni nani aliyefanya sawa na mapenzi ya baba yake?” Wale wakubwa wakajibu: “Ni yule wa kwanza.” Na Yesu akawaambia: “Kweli ninawaambia: Walipishaji wa kodi pamoja na makahaba wataingia mbele yenu katika Ufalme wa Mungu. Kwa maana Yoane alikuja kwenu kuwaonyesha njia ya haki, nanyi hamukumusadiki. Lakini walipishaji wa kodi na makahaba walimusadiki. Na ijapokuwa muliona mambo hayo yote, hamukugeuka toka zambi zenu na kumusadiki.” “Musikilize mufano mwingine. Mutu mumoja alipanda shamba la mizabibu, akalizungusha upango, akatengeneza nafasi ya kukamulia matunda ya mizabibu na kujenga munara kwa ajili ya walinzi wa shamba. Kisha kupatana kwa kugawanyana mavuno na walimaji wamoja watakaobaki wakitunza shamba lake, akaenda safari katika inchi ingine. Wakati siku za mavuno zilipotimia, akawatuma watumishi wake kwa wale walimaji kusudi wamupatie sehemu yake ya mavuno. Lakini wale walimaji wakawakamata wale watumishi. Wakamupiga mumoja, wakamwua mwingine na kumutupia mwingine mawe hata akakufa. Halafu mwenye shamba akatuma tena watumishi wengine wengi zaidi kuliko wale wa kwanza, lakini wale walimaji wakawatendea namna ile ile. Kwa mwisho, akamutuma mwana wake kwao, akisema: ‘Ninajua kwamba watamuheshimu mwana wangu.’ Lakini wakati walimaji walipomwona yule mwana, wakasemezana: ‘Musimame! Huyu ndiye atakayerizi shamba hili. Basi tumwue, na shamba hili litakuwa urizi wetu!’ Basi wakamukamata, wakamwua na kutupa maiti yake inje ya shamba.” Kisha Yesu akauliza: “Basi wakati mwenye shamba la mizabibu atakapokuja, atafanya nini na wale walimaji?” Nao wakamujibu: “Atawaua hao watu wabaya pasipo huruma, naye atapatana na walimaji wengine kwa kutunza shamba lake na kumupatia sehemu yake ya matunda kwa wakati wa mavuno.” Na Yesu akawaambia: “Hamujasoma bado Maandiko Matakatifu yanayosema: ‘Jiwe lililokataliwa na wajengaji limekuwa jiwe kubwa la musingi. Ni Bwana aliyefanya jambo hili, nalo ni ajabu sana kwetu.’ Kwa sababu hii ninawaambia: Ufalme wa Mungu utaondolewa kwenu na kupewa kwa watu watakaotoa matunda yanayostahili ufalme ule. [ Anayeanguka juu ya jiwe hili atavunjikavunjika, na yule litakayemwangukia, atapondekana.]” Wakubwa wa makuhani na Wafarisayo waliposikia mifano hiyo Yesu aliyoitumia, wakatambua kwamba alisema juu yao. Kwa hiyo wakatafuta kumukamata, lakini waliogopa makundi ya watu kwa sababu wao walisadiki kwamba yeye ni nabii. Yesu akaendelea kusema na lile kundi la watu kwa mifano. Akawaambia: “Ufalme wa mbinguni unafanana na mufalme mumoja aliyemufanyia mwana wake karamu ya ndoa. Yeye akawatuma watumishi wake kwa kuwaita watu wale walioalikwa kwa karamu, lakini hawakutaka kufika. Kisha akawatuma watumishi wengine, akisema: ‘Mwende kuwaambia waalikwa kwamba karamu yangu iko sasa tayari. Nimechinja ngombe na nyama wenye kunona; vitu vyote viko tayari. Muwaambie wafike kwa karamu!’ Lakini wale waalikwa hawakushugulika na aliko lake; wakajiendea: mumoja kwenye shamba lake, mwingine kwenye biashara yake, na wengine wakawakamata wale watumishi wakawatesa na kuwaua. Halafu mufalme akakasirika. Akawatuma waaskari wake kuwaua wale wauaji na kuteketeza muji wao kwa moto. Kisha akawaambia watumishi wake: ‘Karamu ya ndoa iko tayari, lakini si wale walioalikwa ndio waliostahili kuikula. Basi muende kwenye masanganjia, na watu wote mutakaowaona, muwaalike wafike kwa karamu.’ Nao watumishi wakaenda katika barabara, wakakusanya watu wote waliowaona, wabaya na wazuri, na nyumba ya karamu ikajaa na wageni. “Naye mufalme alipoingia kwa kuwaangalia wale wageni, akamwona mutu mumoja asiyevaa nguo ya karamu. Akamwuliza: ‘Rafiki, namna gani umeingia hapa bila kuvaa nguo ya karamu?’ Lakini yule mutu hakumujibu neno. Halafu mufalme akawaambia watumishi wake: ‘Mumufunge mutu huyu miguu na mikono na kumutupa inje kwenye giza. Kule atalia na kusaga meno.’ ” Kisha, Yesu akasema: “Watu wanaoitwa ni wengi, lakini wale wanaochaguliwa ni wachache.” Wafarisayo walienda kufanya shauri kusudi wapate kumunasa Yesu katika masemi. Halafu wakatuma kwake wamoja kati ya wanafunzi wao pamoja na watu wengine wamoja waliojiunga na Herode kumwuliza maneno haya: “Mwalimu, tunajua kuwa wewe ni mutu wa kweli na kwamba unafundisha kwa kweli njia Mungu anayoamuru. Vilevile haushuguliki na mafikiri ya mutu yeyote kwa sababu hauangalii cheo cha mutu. Basi utuambie unafikiri nini: Sheria yetu inaturuhusu kulipa kodi kwa Mufalme wa Roma au hapana?” Lakini kwa kuwa Yesu alijua makusudi yao mabaya, akawajibu: “Ninyi wanafiki, kwa sababu gani munanipima? Munionyeshe feza inayotolewa kwa kulipa kodi.” Basi wakamuletea kikoroti kimoja cha feza. Yesu akawauliza: “Sura hii na jina hili linaloandikwa hapa ni vya nani?” Wakamujibu: “Ni vya Mufalme wa Roma.” Halafu Yesu akawaambia: “Basi mumupe Mufalme wa Roma vinavyokuwa vyake, na Mungu vinavyokuwa vyake.” Nao waliposikia jibu hili, wakashangaa sana, wakamwacha Yesu na kujiendea. Siku ile ile, Wasadukayo wamoja wakamufikia Yesu. (Watu hawa ndio wanaosema kwamba wafu hawatafufuka.) Wakamwuliza: “Mwalimu, Musa alisema: ‘Mutu akikufa bila kuacha mutoto, ndugu yake anapaswa kumwoa yule mujane na kumuzalia marehemu watoto.’ Basi huku kwetu kulikuwa wandugu saba. Wa kwanza alioa mwanamuke, kisha akakufa bila kuzaa mutoto. Naye akamwachia ndugu yake yule mwanamuke. Na ikakuwa vile kwa ndugu wa pili na wa tatu na mpaka yule wa saba. Nyuma ya kufa kwa wote saba, yule mwanamuke akakufa vilevile. Sasa, siku wafu watakapofufuka, muke yule atakuwa wa nani, kwa maana wote saba walikuwa wamemwoa?” Yesu akawajibu: “Munadanganyika, kwa sababu ya kutojua Maandiko Matakatifu wala uwezo wa Mungu. Kwa maana wakati wafu watakapofufuka wataishi kama vile wamalaika wanavyoishi katika mbingu; hawataoa wala kuolewa. Na juu ya kufufuka kwa wafu, hamujasoma bado maneno haya Mungu aliyowaambia? ‘Mimi ni Mungu wa Abrahamu, Mungu wa Isaka na Mungu wa Yakobo.’ ” Yesu akaendelea kuwaambia: “Mungu si Mungu wa waliokufa, lakini ni Mungu wa wanaokuwa wazima.” Makundi ya watu waliposikia maneno hayo, wakashangaa sana na mafundisho yake. Wafarisayo waliposikia kwamba Yesu aliwafungisha Wasadukayo kinywa, wakakusanyika pamoja. Na mumoja wao, aliyekuwa mwalimu mukubwa wa Sheria, akamufikia Yesu na kumwuliza hivi kwa kumupima: “Mwalimu, katika Sheria, ni amri gani inayokuwa kubwa katikati ya zote?” Yesu akamujibu: “ ‘Umupende Bwana Mungu wako kwa moyo wako wote, kwa roho yako yote na kwa akili yako yote.’ Hii ndiyo amri inayokuwa kubwa zaidi, na ya kwanza. Na ya pili inayofanana nayo ni hii: ‘Umupende mwenzako kama vile unavyojipenda mwenyewe.’ Amri hizi mbili ndicho kifungo cha Sheria yote ya Musa na mafundisho ya manabii.” Kwa kuona vile Wafarisayo walivyokuwa wamekusanyika, Yesu akawauliza: “Munafikiri nini juu ya Kristo? Yeye ni mwana wa nani?” Nao wakamujibu: “Yeye ni mwana wa Daudi.” Na Yesu akawaambia: “Basi namna gani Daudi, akiongozwa na Roho, aliweza kumwita ‘Bwana’, akisema: ‘Bwana wetu Mungu alimwambia Bwana wangu: Ikaa na mamlaka kwa kuume kwangu mpaka nitakapoweka waadui zako chini ya miguu yako.’ “Basi ikiwa Daudi anamwita Kristo ‘Bwana,’ namna gani Kristo anaweza kuwa mwana wake?” Basi hakuna mutu aliyeweza kumujibu neno, na tangia siku ile hakuna aliyesubutu kumwuliza tena neno. Halafu Yesu akawaambia makundi ya watu na wanafunzi wake: “Walimu wa Sheria na Wafarisayo wamepewa madaraka ya kueleza Sheria ya Musa. Basi kwa hiyo munapaswa kuwatii na kushika maneno yote wanayowaambia; lakini musifuate matendo yao, kwa maana mambo wanayoyasema, si ndiyo wanayofanya. Wanafunga mizigo mizito na kuibebesha watu wengine kwa mabega, lakini wao wenyewe hawafikiri hata kidogo juu ya namna ya kuwasaidia kuibeba. Wanafanya matendo yao yote tu kusudi wajionyeshe mbele ya watu. Wanajifungia kwa paji za nyuso vibweta vipana vyenye vikaratasi vya Maandiko Matakatifu. Nao wanavaa kanzu zenye pembe ndefu. Wanapenda kuikaa kwenye nafasi za heshima katika karamu na katika viti vya mbele ndani ya nyumba za kuabudia. Wanapenda vilevile kusalimiwa kwa heshima kwenye nafasi za makutano, na kuitwa ‘Mwalimu.’ Lakini ninyi musikubali kuitwa ‘Mwalimu’, kwa maana ninyi wote ni wandugu, nanyi muko na Mwalimu mumoja tu. Vilevile hapa katika dunia musimwite mutu yeyote ‘Baba’ kwa maana muko na Baba mumoja tu, anayekuwa mbinguni. Musikubali kuitwa ‘Waongozi,’ kwa maana muko na Mwongozi Mukubwa mumoja tu, ndiye Kristo. Lakini anayekuwa mukubwa kati yenu sherti akuwe mutumishi wenu. Na yeyote anayejiinua, atashushwa, lakini anayejishusha, atainuliwa. “Ole kwenu, ninyi walimu wa Sheria na Wafarisayo, ninyi wanafiki! Munawafungia watu wengine njia ya kuingia katika Ufalme wa mbinguni. Ninyi wenyewe hamwingii mule na zaidi ya hii munawazuiza wale wanaotaka kuingia. [ “Ole kwenu, ninyi walimu wa Sheria na Wafarisayo, ninyi wanafiki! Munanyanganya mali za wajane na kuomba maombi marefu kwa kujionyesha. Kwa sababu hii azabu yenu itakuwa kubwa zaidi!] “Ole kwenu, ninyi walimu wa Sheria na Wafarisayo, ninyi wanafiki! Munasafiri kuvuka bahari na inchi mbalimbali kusudi mupate kumugeuza hata mutu mumoja tu kuwa mufuasi wenu. Nanyi munapomupata, munamufanya kuwa mwenye kustahili azabu ya jehenamu mara mbili zaidi kuliko ninyi. “Ole kwenu, ninyi waongozi vipofu! Ninyi munaosema kwamba mutu akiapa kwa jina la hekalu, si kitu; lakini kama akiapa akitaja zahabu inayokuwa ndani ya hekalu, anapaswa kutimiza kiapo chake. Ninyi wapumbafu na vipofu! Ni nini inayokuwa kubwa zaidi, zahabu au hekalu linaloifanya zahabu ile ihesabiwe kuwa takatifu? Munasema vilevile kwamba mutu akiapa akitaja mazabahu, si kitu; lakini kama akiapa akitaja sadaka inayokuwa juu yake, anapaswa kutimiza kiapo chake. Ninyi vipofu! Ni nini inayokuwa kubwa zaidi, sadaka au mazabahu ndiyo inayoifanya sadaka ile ihesabiwe kuwa takatifu? Katika haya yote mutu anayeapa kwa jina la mazabahu anaapa kwa jina lile na kwa majina ya vyote vinavyokuwa juu yake. Vilevile anayeapa kwa jina la hekalu anaapa kwa jina lile na kwa jina la Mungu anayekuwa ndani yake. Naye anayeapa kwa jina la mbingu anaapa kwa jina la kiti cha kifalme cha Mungu na kwa jina la Mungu anayeikaa juu yake. “Ole kwenu, ninyi walimu wa Sheria na Wafarisayo, ninyi wanafiki! Munatoa fungu moja la kumi la vijani vya kukoleza chakula, lakini mumeacha mambo makubwa yanayoamuriwa na Sheria, kama vile haki, huruma, na uaminifu. Mambo hayo ndiyo muliyopaswa kushika pasipo kuacha mengine. Ninyi waongozi vipofu! Munapokunywa, munachuya inzi toka katika vinywaji vyenu, lakini munameza ngamia! “Ole kwenu, ninyi walimu wa Sheria na Wafarisayo, ninyi wanafiki! Ninyi ni kama mutu anayesafisha tu inje ya kikombe na sahani, lakini ndani kumejaa vitu mulivyovipata kwa njia ya wizi na tamaa mbaya. Wewe kipofu Mufarisayo! Safisha kwanza ndani ya kikombe na ya sahani, na kisha inje yake kutakuwa safi vilevile. “Ole kwenu, ninyi walimu wa Sheria na Wafarisayo, ninyi wanafiki! Munafanana na makaburi yaliyopakaliwa chokaa, yanayoonekana kuwa mazuri kwa inje, lakini ndani yanajaa mifupa ya wafu na uchafu wa kila namna. Ni vile ninyi munavyokuwa, kwa inje munaonekana kuwa wenye haki mbele ya watu, lakini ndani yenu munajaa unafiki na uovu. “Ole kwenu, ninyi walimu wa Sheria na Wafarisayo, ninyi wanafiki! Munajenga makaburi ya manabii na kupamba makaburi ya watu waliokuwa wema. Nanyi munasema: ‘Kama sisi tungaliishi katika nyakati za babu zetu, hatungalijiunga nao katika shauri la kuwaua manabii.’ Hivi munajishuhudia ninyi wenyewe kuwa ninyi ni ukoo wa watu waliowaua manabii. Basi mutimize hayo mambo babu zenu waliyoyaanza! Ninyi kikundi cha nyoka! Namna gani mutaweza kuepuka azabu ya jehenamu? Kwa sababu hiyo, nitawatumia manabii na watu wenye hekima na walimu. Mutawaua wamoja wao, mutatundika wengine juu ya misalaba, mutawapiga wengine fimbo ndani ya nyumba zenu za kuabudia na kuwafukuza muji kwa muji. Na hivi mutabeba lazima ya damu iliyomwangwa katika dunia pasipo kosa, tangia kuuawa kwa Abeli aliyekuwa mukamilifu mpaka kuuawa kwa Zakaria, mwana wa Barakia, muliyemwuia kwenye hekalu katikati ya Pahali Patakatifu na mazabahu. Kweli ninawaambia: watu wa kizazi hiki watabeba lazima ya mambo hayo yote. “Ewe Yerusalema, Ewe Yerusalema. Wewe unaua manabii na kuwatupia mawe wale ambao Mungu anakutumia. Mara nyingi nilitaka kuwakusanya wakaaji wako kama vile kuku anavyokusanya vitoto vyake chini ya mabawa yake, lakini ninyi hamukutaka! Angalia, makao yenu yanaachwa ukiwa. Kwa maana ninawaambia, tangia sasa hamutaniona tena mpaka mutakaposema: ‘Abarikiwe huyu anayekuja kwa jina la Bwana.’ ” Yesu akatoka ndani ya hekalu, na alipokuwa akienda, wanafunzi wake wakamufikia na kumwonyesha majengo ya hekalu. Lakini Yesu akawaambia: “Munaona haya yote? Kweli ninawaambia: hapa hakutabaki hata jiwe moja juu ya lingine; yote yatabomolewa.” Basi Yesu alipokuwa akiikaa kwa mulima wa Mizeituni, wanafunzi wake wakamwendea peke yao na kumwuliza: “Utuambie, mambo hayo uliyotoka kusema yatakuwa wakati gani? Na kitambulisho cha kurudi kwako nao wakati wa mwisho wa dunia ni nini?” Yesu akawajibu: “Muangalie vizuri, mutu asiwadanganye. Watu wengi watakuja wakijiita kwa jina langu, wakisema: ‘Mimi ni Kristo!’ Nao watawadanganya wengi. Mutasikia habari za matokeo au utetezi wa vita, lakini musiogope. Sherti mambo hayo yatukie, lakini hayaonyeshi kama mwisho umefika. Kwa maana taifa litapigana na taifa, na ufalme utapigana na ufalme. Kutakuwa njaa na tetemeko ya inchi katika pahali mbalimbali. Na haya yote ni kama mwanzo wa maumivu ya kuzaa tu. “Halafu watu watawatoa kusudi muteswe na kuuawa, na watu wa mataifa yote watawachukia ninyi kwa ajili yangu. Kwa wakati ule watu wengi wataanguka katika imani yao; watatoana wao kwa wao na kuchukiana. Manabii wengi wa uongo watatokea, nao watawadanganya watu wengi. Na kwa sababu ya kuongezeka kwa maovu, upendo wa watu wengi utapunguka. Lakini atakayevumilia mpaka mwisho ataokolewa. Na hii Habari Njema ya Ufalme itahubiriwa katika dunia nzima kuwa ushuhuda kwa mataifa yote; na halafu mwisho wa dunia utatimia. “Mutamwona yeye anayeitwa ‘Chukizo Linaloleta Uharibifu,’ yule aliyetajwa na nabii Danieli, akisimamishwa katika hekalu. (Anayesoma maneno haya aelewe maana yake.) Basi watakaokuwa Yudea, wakimbilie kwa milima. Atakayekutiwa juu ya paa la nyumba asishuke ndani yake kwa kutwaa kitu. Na mutu atakayekutiwa katika shamba, asirudi kwake kwa kutwaa nguo yake. Wanawake wenye mimba na wenye kunyonyesha watapata hasara katika siku zile! Mumwombe Mungu kusudi kukimbia kwenu kusikuwe wakati wa mvua au kwa siku ya Sabato! Kwa maana katika siku zile kutakuwa mateso makubwa yasiyotokea tangia kuumbwa kwa dunia mpaka sasa, wala hakutatokea tena mateso kama yale. Na kama Mungu asingepunguza siku zile za mateso, hakuna hata mutu mumoja angeponyoka kufa. Lakini kwa ajili ya watu wake aliowachagua, yeye atazipunguza. “Kwa wakati ule mutu akiwaambia ninyi: ‘Angalia, Kristo yuko hapa!’ au ‘Yuko kule!’, musimusadiki kwa maana kutatokea watu wanaojiita kwa uongo ‘Kristo’ pamoja na manabii wa uongo, nao wataonyesha vitambulisho vikubwa na maajabu, hata ikiwezekana, wawadanganye hata watu waliochaguliwa na Mungu. Angalia, nimewaambia haya yote mbele. “Basi kama watu wakiwaambia: ‘Angalia, Kristo yuko katika jangwa!’, musiende kule. Au wakiwaambia: ‘Angalia, yuko katika chumba cha ndani!’, musiwasadiki. Kwa maana kama vile umeme unavyoangaza na kuonekana katika mbingu yote, ni vile Mwana wa Mutu atakavyoonekana siku atakapokuja. “Nafasi yoyote kunapokuwa muzoga, ndipo tai wanapokusanyika. “Mara moja kisha mateso ya siku zile, jua litatiwa giza, mwezi hautaangaza, nyota zitaanguka toka mbinguni na vyote vyenye nguvu katika mbingu vitatikiswa. Kisha kitambulisho cha kurudi kwa Mwana wa Mutu kitaonekana katika mbingu. Nayo mataifa yote ya dunia yatakuwa katika malalamiko, na yatamwona Mwana wa Mutu akikuja katikati ya mawingu toka mbinguni, kwa uwezo na utukufu mukubwa. Baragumu kubwa itapigwa, halafu atawatuma wamalaika wake katika pande ine za dunia, kusudi wawakusanye watu wake aliowachagua, kutoka katika dunia nzima. “Muangalilie mufano juu ya muti wa tini. Wakati matawi yake yanapochipuka, nayo majani yao yanapochipuka, ninyi munatambua kwamba wakati wa jua kali unakaribia. Vilevile, wakati mutakapoona mambo haya yote niliyotoka kutaja yanatokea, mujue kwamba yeye yuko karibu, na amekuwa kwa mulango. Maana kweli ninawaambia: hiki kizazi hakitapita mbele ya kutimia kwa mambo hayo yote. Mbingu na dunia vitatoweka, lakini maneno yangu hayatabadilika hata kidogo. “Lakini hakuna mutu anayejua siku ile na saa, hata wamalaika wa mbinguni, hata Mwana, isipokuwa Baba peke yake tu. Kama ilivyokuwa katika siku za Noa, ndivyo itakavyokuwa wakati Mwana wa Mutu atakaporudi. Kwa maana katika siku zile mbele ya kunyesha kwa mvua kubwa, watu walikuwa wakikula na kunywa, wakioa na kuolewa, mpaka ilipotimia siku ile Noa alipoingia ndani ya chombo. Nao hawakutambua kitu mpaka mvua kubwa sana ilipotokea, na kuwaua wote. Na ni hivi itakavyokuwa wakati Mwana wa Mutu atakaporudi. Wakati ule, watu wawili watakutiwa katika shamba moja; mumoja atapelekwa na mwingine ataachwa. Wanawake wawili watakutiwa wakisaga pamoja, mumoja atapelekwa na mwingine ataachwa. Basi mukeshe, kwa sababu hamujui siku Bwana wenu atakaporudi. Munajua vema kwamba mwenye nyumba angalijua wakati gani mwizi atakapokuja kuiba, angalikesha na kuchunga nyumba yake isibomolewe. Kwa hiyo, ninyi vilevile mukuwe tayari, kwa sababu Mwana wa Mutu atarudi saa musiyozania. “Basi ni nani anayekuwa mutumishi mwaminifu na mwenye akili? Ni yule bwana wake aliyemuweka kuwa musimamizi wa watumishi wake wengine na kumwamuru kuwapatia posho yao kwa wakati uliopangwa. Heri mutumishi yule ikiwa saa bwana wake anaporudi, anamukuta akifanya kazi ile. Kweli ninawaambia: bwana wake atamuweka mutumishi yule kuwa musimamizi wa mali yake yote. Lakini kama mutumishi yule ni mutu mubaya, atajisemesha yeye mwenyewe kwamba bwana wake anakawia, naye ataanza kuwapiga watumishi wenzake, na kula na kunywa pamoja na walevi. Basi bwana wa mutumishi yule atakuja siku asiyozania na saa asiyojua. Naye atamupiga vikali na atamwazibu sawa na watu wanafiki, akimuweka kwenye nafasi atakapolia na kusaga meno. “Halafu kwa wakati ule, Ufalme wa mbinguni utafanana na wabinti kumi waliotwaa taa zao na kwenda kumupokea bwana-arusi. Watano kati yao walikuwa wajinga na watano walikuwa wenye akili. Wale wajinga walitwaa taa zao tu, lakini hawakupeleka mafuta ya kutia ndani yao. Lakini wale wenye akili walitwaa machupa ya mafuta pamoja na taa zao. Na kwa kuona bwana-arusi alikawia kufika, wote wakasinzia na kulala usingizi. “Ilipokuwa katikati ya usiku, kelele likasikilika, likisema: ‘Angalia, bwana-arusi anakuja! Muondoke kwenda kumupokea!’ Halafu wale wabinti kumi wakaamuka, wakatengeneza taa zao. Wale wajinga wakawaambia wenye akili: ‘Mutusaidie na mafuta kidogo, kwa sababu taa zetu zinaanza kuzimika.’ Lakini wale wenye akili wakajibu: ‘Haiwezekani, mafuta tunayokuwa nayo hayatutoshelei. Afazali muende kwa wachuuzi na kujinunulia yenu.’ Wale wajinga walipokwenda kununua mafuta, bwana-arusi akafika. Wale wenzao watano waliokuwa tayari wakaingia pamoja naye katika karamu ya ndoa. Kisha mulango ukafungwa. “Nyuma, hao wengine wakafika, na kuanza kusema: ‘Bwana, bwana, utufungulie!’ Lakini bwana akajibu: ‘Kweli ninawaambia: mimi siwajui ninyi.’ ” Na Yesu akaongeza kusema: “Basi mukeshe, kwa sababu hamujui siku wala saa ile. “Maana mambo hayo ya Ufalme wa mbinguni ni kama mutu aliyetaka kwenda safari. Yeye akawaita watumishi wake, akawagawanyia mali yake. Akamupatia mumoja furushi tano za zahabu, mwingine furushi mbili na mwingine furushi moja kwa kadiri ya uwezo wa kila mumoja, kisha akasafiri. Mara moja yule mutumishi aliyepata furushi tano, akaenda kufanya uchuuzi na mali ile, akafaidia zingine tano. Na yule aliyepata furushi mbili akafaidia zingine mbili. Lakini yule aliyepewa furushi moja, akachimba shimo katika udongo na kuficha ile mali ya bwana wake mule. “Kulipopita siku nyingi, bwana wa watumishi wale akarudi, akafanya hesabu ya mali yake pamoja nao. Yule mutumishi aliyepewa furushi tano za zahabu, akakuja, akaleta faida ya zingine tano. Na akasema: ‘Bwana, umenipatia furushi tano za zahabu, na sasa angalia, kuna faida ya zingine tano.’ Bwana wake akamwambia: ‘Ni vizuri, wewe mutumishi mwema na mwaminifu. Ulikuwa mwaminifu katika ulinzi wa mali ndogo, basi nitakuweka kuwa mulinzi wa mali mengi. Kuja ufurahi pamoja na bwana wako.’ Halafu mutumishi aliyepewa furushi mbili akakuja, akasema: ‘Bwana, umenipatia furushi mbili; na sasa angalia, kuna faida ya zingine mbili.’ Bwana wake akamwambia: ‘Ni vizuri, wewe mutumishi mwema na mwaminifu. Ulikuwa mwaminifu katika ulinzi wa mali ndogo, basi nitakuweka kuwa mulinzi wa mali mingi. Kuja ufurahi pamoja na bwana wako!’ Kisha yule mutumishi aliyepewa furushi moja akakuja, akasema: ‘Bwana, nilijua kuwa wewe ni mutu mugumu anayevuna nafasi asipopanda, na kukusanya nafasi asiposambaza. Kwa hiyo niliogopa, nami nikaenda kuficha ile mali yako ndani ya udongo. Basi mali yako ndiyo hii, uitwae.’ Naye bwana wake akamujibu: ‘Wewe mutumishi mubaya na muvivu! Ulijua kama ninavuna nafasi nisipopanda, na kukusanya nafasi nisiposambaza. Basi, ungepaswa kuweka mali yangu ndani ya banki, kusudi siku ya kurudi kwangu, ningepata mali yangu pamoja na faida yake. Mumunyanganye ile furushi moja na kuitoa kwa yule anayekuwa na furushi kumi. Kwa maana mutu anayekuwa na kitu ataongezewa kingine; lakini mutu asiyekuwa na kitu, ataondolewa hata kidogo anachokuwa nacho. Na zaidi ya hii, mumutupe huyu mutumishi asiyekuwa na mafaa inje kwenye giza. Kule atalia na kusaga meno.’ “Wakati Mwana wa Mutu atakapokuja katika utukufu wake pamoja na wamalaika wote, ataikaa juu ya kiti chake cha kifalme chenye utukufu. Mataifa yote yatakusanyika mbele yake, naye atayatenga kwa makundi mawili kama vile muchungaji anavyotenga kondoo na mbuzi. Ataweka kondoo kwa upande wake wa kuume, na mbuzi kwa upande wake wa kushoto. Halafu mufalme atawaambia wale wanaokuwa kwa upande wake wa kuume: ‘Mukuje, ninyi muliobarikiwa na Baba yangu; muingie katika Ufalme muliotayarishiwa tangu kuumbwa kwa dunia. Kwa maana nilisikia njaa, mukanipa chakula; nilisikia kiu, mukanipa maji; nilikuwa mugeni, mukanikaribisha; nilikuwa uchi, mukanipatia nguo; nilikuwa mugonjwa, mukanisaidia; nilikuwa katika kifungo, mulikuja kuniangalia.’ Halafu wenye haki watamujibu: ‘Bwana, ni wakati gani tulipokuona ukisikia njaa, tukakupa chakula, au uliposikia kiu, tukakupa maji? Ni wakati gani tulipokuona uko mugeni, tukakukaribisha, ulipokuwa uchi, tukakupatia nguo? Na ni wakati gani tulipokuona uko mugonjwa au uko katika kifungo tukakuja kukuangalia?’ Mufalme atawajibu: ‘Kweli ninawaambia: kila kitu mulichokitendea mumoja wa hawa wandugu zangu wanaohesabiwa kuwa wadogo, mulinitendea mimi.’ “Kisha mufalme atawaambia wale wanaokuwa kwa upande wake wa kushoto: ‘Muondoke hapa karibu nami, ninyi muliolaaniwa! Muende katika moto usiozimika hata milele, uliotayarishwa kwa ajili ya Shetani na wamalaika wake! Kwa maana nilisikia njaa, nanyi hamukunipa chakula; nilisikia kiu, nanyi hamukunipa maji; nilikuwa mugeni, nanyi hamukunikaribisha; nilikuwa uchi, nanyi hamukunipatia nguo; nilikuwa mugonjwa na nilikuwa katika kifungo, nanyi hamukukuja kuniangalia.’ Halafu nao watajibu: ‘Bwana, ni wakati gani tulipokuona ukisikia njaa, au kiu, au ukikuwa mugeni, au uchi, au mugonjwa, au mufungwa, nasi hatukukusaidia?’ Naye mufalme atawajibu: ‘Kweli ninawaambia: kila kitu mulichokosa kumutendea mumoja wa hawa wanaohesabiwa kuwa wadogo, hamukunitendea mimi.’ Halafu hawa watakwenda kwenye nafasi watakapoazibiwa kwa milele, lakini wenye haki wataingia kwenye uzima wa milele.” Yesu alipomaliza kusema maneno hayo yote, akawaambia wanafunzi wake: “Munajua kwamba kumebaki siku mbili mbele ya kutimia kwa sikukuu ya Pasaka, na Mwana wa Mutu apate kutolewa kusudi atundikwe juu ya musalaba.” Wakubwa wa makuhani na wasimamizi wa watu wakakusanyika ndani ya nyumba ya Kuhani Mukubwa, aliyeitwa Kayafa, nao wakafanya shauri la kumukamata Yesu kwa werevu na kumwua. Lakini walijisemesha: “Tusimukamate kwa wakati wa karamu, kusudi fujo isitokee kati ya watu.” Yesu alipokuwa Betania katika nyumba ya mutu aliyeitwa Simoni Mukoma, mwanamuke mumoja aliingia ndani ya nyumba, akiwa na chupa la jiwe lenye kuwa na marasi ya bei kali, akaimimia juu ya kichwa cha Yesu walipokuwa wakikula. Wanafunzi wake walipoona jambo lile, wakachukizwa na kusema: “Kwa nini kupoteza mali namna hii? Marasi hii ingeuzishwa kwa bei kali na kuwagawanyia wamasikini mali ile!” Lakini Yesu akatambua mawazo yao na kuwaambia: “Sababu gani munamusumbua mwanamuke huyu? Amenitendea jambo zuri. Kwa maana mutakuwa na wamasikini pamoja nanyi siku zote, lakini mimi sitakuwa pamoja nanyi siku zote. Mwanamuke huyu amemimia marasi hii juu ya mwili wangu kwa kuutayarisha kwa ajili ya maziko. Kweli ninawaambia: kwa ajili ya kukumbuka mwanamuke huyu, tendo lile alilofanya litaelezwa popote Habari Njema hii itakapohubiriwa katika dunia nzima.” Halafu mumoja wa wanafunzi kumi na wawili, aliyeitwa Yuda Iskariota, akaenda kwa wakubwa wa makuhani na kuwaambia: “Mutanipa nini kama nikimutoa Yesu kwenu?” Basi wakamupa vikoroti makumi tatu vya feza. Tangia wakati ule Yuda akaanza kutafuta wakati unaokuwa muzuri kwa kumutoa. Siku ya kwanza ya karamu ya sikukuu ya Mukate Usiotiwa Chachu, wanafunzi wakamwendea Yesu na kumwuliza: “Ni wapi unapotaka tukutayarishie karamu ya Pasaka?” Yesu akawaambia kwamba waende katika muji kwa mutu mumoja na kumwambia: “Mwalimu anasema: ‘Siku yangu inakaribia. Mimi na wanafunzi wangu tutakula karamu ya Pasaka kwako.’ ” Nao wanafunzi wakafanya sawa Yesu alivyowaagiza, wakatayarisha karamu ya Pasaka. Ilipokuwa magaribi, Yesu akaikaa kula chakula pamoja na wanafunzi wake kumi na wawili. Nao walipokuwa wakikula, akasema: “Kweli ninawaambia: mumoja kati yenu atanitoa.” Wanafunzi wakahuzunika sana na kuanza kumwuliza mumoja kwa mumoja: “Bwana, ni mimi?” Yesu akajibu: “Yule aliyechovya mukate pamoja nami ndani ya sahani ndiye atanitoa. Mwana wa Mutu atakufa sawa vile Maandiko Matakatifu yanavyosema juu yake, lakini ole kwa mutu yule atakayemutoa! Ingekuwa heri kwake kama asingezaliwa!” Halafu Yuda, aliyemutoa, akamwuliza: “Mwalimu, ni mimi?” Naye Yesu akamujibu: “Wewe umesema.” Walipokuwa wakikula, Yesu akatwaa mukate, akaubariki, kisha akaumega na kuwapa wanafunzi wake, akisema: “Mutwae na mukule, huu ni mwili wangu.” Kisha akatwaa kikombe, akakibariki na kuwapa, akisema: “Mukunywe ninyi wote, kwa maana hii ni damu yangu inayomwangika kwa ajili ya wengi kusudi wasamehewe zambi. Nayo damu hii inahakikisha agano la Mungu. Nami ninawaambia kwamba tangia sasa sitakunywa tena divai mpaka siku ile nitakapoikunywa mupya pamoja nanyi katika Ufalme wa Baba yangu.” Nao walipokwisha kuimba, wakaondoka kwenda kwa mulima wa Mizeituni. Halafu Yesu akawaambia wanafunzi wake: “Usiku huu ninyi wote mutaanguka kwa ajili yangu, kwa maana imeandikwa hivi katika Maandiko Matakatifu: ‘Nitamwua muchungaji, na kondoo wa kundi watasambazwa.’ Lakini nitakapokwisha kufufuka, nitawatangulia Galilaya.” Petro akamujibu: “Hata wote wakianguka, mimi sitaanguka hata kidogo.” Yesu akamujibu: “Kweli ninakuambia kwamba katika usiku huu, mbele jogoo hajawika utakuwa umenikana mara tatu.” Lakini Petro akamwambia: “Hata ikinipasa kufa pamoja nawe, sitakukana hata kidogo.” Na wanafunzi wote wengine wakasema sawasawa naye. Kisha Yesu pamoja na wanafunzi wake wakafika katika bustani inayoitwa Getesemane. Na Yesu akawaambia: “Muikae hapa, kwa wakati ninapokwenda kuomba kule.” Na akatwaa Petro na wana wawili wa Zebedayo na kwenda nao. Akaanza kuhuzunika na kuhangaika. Halafu akawaambia: “Ninahuzunika sana, karibu kufa! Mubakie hapa na mukeshe pamoja nami.” Kisha akajitenga mbali kidogo nao, akainama uso chini. Akaomba akisema: “Ee Baba yangu, kama ikiwezekana, ninakuomba uniondolee mbali kikombe hiki cha mateso. Lakini isikuwe kama vile mimi ninavyotaka, lakini kama vile wewe unavyotaka.” Kisha akarudi pahali pale alipowaacha wale wanafunzi, akawakuta wamelala usingizi. Akamwambia Petro: “Hamukuweza kukesha pamoja nami hata kwa saa moja tu? Mukeshe na muombe, kusudi musianguke katika majaribu; kwa maana roho ni hodari, lakini mwili ni zaifu.” Akawaacha tena kwa mara ya pili, akaomba akisema: “Ee Baba yangu, kama kikombe hiki cha mateso hakiwezi kupita mbali nami, bila mimi kukikunywa, basi mapenzi yako yafanyike!” Aliporudi tena, akawakuta wanafunzi wale wamelala usingizi, kwa maana macho yao yalikuwa yamewezwa sana na usingizi. Yesu akawaacha tena, na kwenda kuomba kwa mara ya tatu, akirudilia maombi yale yale. Kisha akarudi kwenye wanafunzi wake na kuwaambia: “Mungali munalala na kupumzika? Angalia, saa imetimia, sasa Mwana wa Mutu anatolewa katika mikono ya wenye zambi. Musimame, tuende! Angalia, yule anayenitoa amefika karibu!” Yesu alipokuwa hajamaliza kusema, Yuda, mumoja wa wanafunzi kumi na wawili, akafika pamoja na kundi kubwa la watu wenye panga na magongo. Hawa wote walikuwa wametumwa na wakubwa wa makuhani na wasimamizi wa watu. Yuda, yule aliyekuwa amemutoa, aliwapa kitambulisho hiki: “Yule nitakayemubusu ndiye yeye, mumukamate.” Yuda alipofika, akamujongelea Yesu, na kumwambia: “Jambo, Mwalimu.” Na kisha akamubusu. Lakini Yesu akamwambia: “Rafiki, ufanye lililokuleta.” Halafu watu wale wakajongea na kumukamata Yesu na kumufunga. Na mumoja wa wale waliokuwa pamoja na Yesu akachomoa upanga wake, akamupiga mutumishi wa Kuhani Mukubwa, akamukata sikio. Halafu Yesu akamwambia: “Rudisha upanga wako katika kifuko chake, kwa maana yeyote anayetumia upanga, atauawa kwa upanga. Haujui kwamba ninaweza kumwomba Baba yangu musaada na mara moja angenitumia zaidi ya makundi kumi na mawili ya wamalaika? Lakini namna gani yangetimia Maandiko Matakatifu yanayosema kwamba mambo haya yanapaswa kuwa hivi?” Kisha Yesu akawaambia watu wale: “Mumekuja na panga na magongo kwa kunikamata kama watu wanavyokwenda kumukamata munyanganyi? Siku zote niliikaa ndani ya hekalu, nikifundisha, nanyi hamukunikamata. Mambo haya yote yamefanyika kusudi maneno yanayosemwa na manabii katika Maandiko Matakatifu yapate kutimia.” Basi wanafunzi wake wote wakamwacha na kukimbia. Wale waliomukamata Yesu wakamupeleka kwa Kuhani Mukubwa Kayafa, pahali walimu wa Sheria na wasimamizi wa watu walipokuwa wamekusanyika. Lakini Petro akamufuata Yesu kwa mbali, hata akaingia ndani ya upango wa Kuhani Mukubwa. Akaingia katika kiwanja, akaikaa pamoja na walinzi kusudi aone mambo yatakayotokea. Wakubwa wa makuhani na wakubwa wote wa Baraza Kubwa walitafuta mashitaki ya uongo juu ya Yesu, kusudi wapate kumwua. Lakini hawakupata neno, ijapokuwa watu wengi walikuja kumusingizia maneno ya uongo. Mwisho watu wawili wakafika na kusema: “Mutu huyu alisema kwamba anaweza kubomoa hekalu la Mungu na kulijenga tena kwa muda wa siku tatu.” Kuhani Mukubwa akasimama na kumwuliza Yesu: “Haujibu hata neno? Watu hawa wanakushitakia nini?” Lakini Yesu akanyamaza. Kuhani Mukubwa akamwambia: “Ninakuapisha kwa jina la Mungu Mwenye Uzima, utuambie kama wewe ndiwe Kristo, Mwana wa Mungu.” Yesu akamujibu: “Wewe umesema. Lakini zaidi ya hiyo, ninawaambia ninyi kwamba mutamwona Mwana wa Mutu akiikaa na mamlaka karibu na Mungu Mwenye Uwezo. Mutamwona vilevile akikuja katika mbingu katikati ya mawingu!” Halafu Kuhani Mukubwa akapasua nguo zake na kusema: “Mutu huyu amemutukana Mungu! Hatuhitaji tena ushuhuda wowote juu yake. Angalia, munatoka kusikia jinsi alivyomutukana Mungu. Munawaza nini?” Nao wakajibu: “Anastahili kufa.” Halafu wamoja wakamutemea mate juu ya uso, na kumupiga ngumi. Na wengine wakamupiga makofi, wakisema: “Ewe Kristo, tambua ni nani aliyekupiga!” Wakati ule Petro alikuwa akiikaa inje katika kiwanja. Mutumishi mumoja mwanamuke akamufikia na kumwambia: “Wewe vilevile ulikuwa pamoja na Yesu wa Galilaya.” Lakini akakana mbele ya wote waliokuwa pale, akisema: “Sijui maneno unayotaka kusema.” Petro alipotoka inje kwa mulango wa upango, mutumishi mwingine mwanamuke akamwona na kuwaambia wale waliokuwa pale: “Huyu alikuwa pamoja na Yesu wa Nazareti.” Lakini Petro akakana tena akaapa akisema: “Ninaapa ya kuwa simujui mutu huyu!” Nyuma kidogo, wale waliosimama pale, wakamufikia Petro na kumwambia: “Hakika wewe ni mumoja wao, kwa maana hata usemi wako unakutambulisha.” Halafu Petro akaanza kusema: “Nilaaniwe ikiwa ninasema uongo! Ninaapa kwamba simujui mutu huyu!” Na mara moja jogoo akawika, naye Petro akakumbuka maneno yale Yesu aliyomwambia kwamba mbele jogoo hajawika, atakuwa amemukana mara tatu. Basi akatoka inje, akalia kwa uchungu sana. Kulipokucha, wakubwa wote wa makuhani na wasimamizi wa watu wakakata shauri la kumwua Yesu. Wakamufunga, wakamupeleka na kwenda kumutoa kwa liwali Pilato. Basi Yuda, aliyemutoa Yesu, alipoona kwamba Yesu amekwisha kuhukumiwa, akajuta, akawarudishia wakubwa wa makuhani na wasimamizi wa watu vile vikoroti makumi tatu vya feza. Akawaambia: “Nimekosa kwa kumutoa mutu huyu asiyekuwa na kosa auawe.” Lakini wao wakamujibu: “Jambo hilo halituelekei. Ni kazi yako wewe mwenyewe!” Yuda akatupa vile vikoroti ndani ya hekalu, naye akaondoka na kwenda kujitundika. Wakubwa wa makuhani wakaokota zile feza na kusema: “Kufuatana na Sheria yetu hairuhusiwi kuweka feza kama hizi ndani ya sanduku ya hekalu kwa sababu feza hizi ni za damu.” Basi walipokwisha kukata shauri, wakatumia zile feza kwa kununua shamba la Mufinyanzi, kusudi likuwe shamba la kuzikia wageni. Ni kutokana na mambo hayo yote shamba lile linaitwa “Shamba la Damu” hata leo. Halafu yakatimia maneno yaliyosemwa na nabii Yeremia: “Walitwaa vikoroti makumi tatu vya feza kufuatana na bei Waisraeli waliyoipanga juu yake, wakazitumia kwa kununua shamba la Mufinyanzi, sawa vile Bwana alivyoniamuru.” Yesu alipopelekwa mbele ya liwali, yeye akamwuliza: “Wewe ndiwe Mufalme wa Wayuda?” Yesu akamujibu: “Wewe umesema.” Na kisha wakubwa wa makuhani na wasimamizi wa watu wakamushitaki, lakini hakujibu neno. Halafu Pilato akamwuliza tena: “Hausikii mambo haya yote wanayokushitakia?” Lakini Yesu hakumujibu hata juu ya neno moja, hata yule liwali akashangaa sana. Kila sikukuu ya Pasaka, liwali alikuwa na desturi ya kuwafungulia watu mufungwa mumoja wanayemutaka. Na katika siku zile kulikuwa mufungwa mumoja aliyejulikana sana, jina lake Baraba. Nao watu walipokuwa wamekusanyika pamoja, Pilato akawauliza: “Munataka niwafungulie nani kati ya Baraba na Yesu anayeitwa Kristo?” Alisema vile kwa maana alijua kwamba walimutoa Yesu kwake kwa sababu walimwonea wivu tu. Pilato alipokuwa amekwisha kuikaa kwa kuamua maneno, muke wake akamutumia ujumbe huu: “Usijiingize katika maneno ya mutu huyo mwenye haki, kwa sababu usiku niliteseka sana katika ndoto kwa ajili yake.” Lakini wakubwa wa makuhani na wasimamizi wa watu wakawashawishi wale waliokusanyika kwamba waombe Baraba afunguliwe, naye Yesu auawe. Liwali akawauliza: “Munataka niwafungulie nani kati ya watu hawa wawili?” Nao wakamujibu: “Utufungulie Baraba.” Pilato akawauliza tena: “Basi munataka nifanye nini na huyu Yesu anayeitwa Kristo?” Nao wote wakajibu: “Atundikwe juu ya musalaba!” Pilato akawauliza tena: “Yeye alifanya ubaya gani?” Lakini wakazidi kupiga kelele wakisema: “Atundikwe juu ya musalaba!” Basi Pilato alipoona kwamba hataweza kufanya kitu, isipokuwa tu kuongeza fujo, akatwaa maji na kunawa mikono yake mbele ya watu wote, akisema: “Lazima ya damu ya mutu huyu isikuwe juu ya kichwa changu! Maneno haya yanawaangukia.” Nao watu wote wakajibu: “Lazima ya damu ya mutu huyu ikuwe juu ya kichwa chetu na juu ya kichwa cha watoto wetu!” Basi Pilato akawafungulia Baraba, lakini akaamuru wamupige Yesu fimbo na kumutoa kusudi atundikwe juu ya musalaba. Kisha waaskari wa liwali Pilato wakamupeleka Yesu ndani ya upango wa nyumba ya liwali, nalo kundi lao lote wakakusanyika na kumuzunguka. Wakamuvua nguo zake na kumuvalisha kanzu nyekundu. Nao wakasokota taji na tawi lenye miiba na kumuvalisha nalo kwenye kichwa chake. Wakaweka tete katika mukono wake wa kuume, wakapiga magoti mbele yake na kumuchekelea, wakisema: “Jambo, Mufalme wa Wayuda!” Wakamutemea mate, wakatwaa lile tete na kumupiga nalo juu ya kichwa. Walipokwisha kumuchekelea, wakamuvua ile kanzu na kumuvalisha nguo zake. Kisha wakaondoka naye kwenda kumutundika juu ya musalaba. Walipokuwa wakiondoka, wakamwona mutu mumoja wa Kurene, aliyeitwa Simoni; wakamushurutisha abebe musalaba wa Yesu. Na walipofika kwenye pahali palipoitwa Golgota, maana yake, “Kilima cha Mufupa wa Kichwa,” wakamupa Yesu divai iliyochanganywa na kinywaji chenye uchungu sana. Lakini alipoionja, akakataa kuikunywa. Nao walipokwisha kumutundika juu ya musalaba, wakagawanya nguo zake kwa kuzipigia kura. Kisha wakaikaa pale kwa kumuchunga. Juu ya kichwa chake wakaweka tangazo hili kwa kuonyesha sababu ya kuhukumiwa kwake: “Huyu ndiye Yesu, Mufalme wa Wayuda.” Vilevile wanyanganyi wawili walitundikwa juu ya misalaba pamoja na Yesu, mumoja kwa upande wake wa kuume na mwingine kwa upande wa kushoto. Watu waliokuwa wakipita pale walimutukana, na kutikisatikisa vichwa vyao, wakisema: “Wewe uliyetaka kubomoa hekalu na kujenga lingine katika siku tatu, ujiokoe sasa wewe mwenyewe! Kama wewe ni Mwana wa Mungu, ujishushe juu ya musalaba!” Vilevile wakubwa wa makuhani walimuchekelea pamoja na walimu wa Sheria na wasimamizi wa watu, wakisemezana hivi: “Aliokoa wengine, lakini sasa anashindwa kwa kujiokoa yeye mwenyewe! Yeye ni mufalme wa Waisraeli, sasa ajishushe pale juu ya musalaba kusudi nasi tupate kumwamini. Yeye alimutumainia Mungu na alisema kwamba yeye ni Mwana wa Mungu. Ikiwa Mungu anapendezwa naye sasa amwokoe!” Hata wale wanyanganyi waliotundikwa pamoja naye walimutukana vilevile. Tangia saa sita ya muchana, giza lilikuwa katika inchi yote mpaka saa tisa. Ilipokuwa karibu saa tisa, Yesu akalalamika akisema: “Eli, Eli, lama sabaktani,” maana yake, “Mungu wangu, Mungu wangu, kwa nini umeniacha?” Na watu wamoja waliosimama pale walipomusikia wakasema: “Anamwita Elia.” Mara moja, mumoja wao akaenda mbio akatwaa kikausho, akakichovya ndani ya divai yenye kuchacha. Akakifungia juu ya tete, akakipandishia Yesu, kusudi apate kunywa. Lakini wengine wakasema: “Mwache, tuone kama Elia atakuja kumwokoa!” Lakini Yesu, akalalamika tena kwa sauti kubwa na kukata roho. Na saa ile ile pazia la hekalu likapasuka vipande viwili toka juu mpaka chini. Inchi ikatetemeka, mawe makubwa yakapasuka, makaburi yakafunguka, na watakatifu wengi waliokufa zamani wakafufuliwa. Wakatoka ndani ya makaburi, na nyuma ya kufufuka kwa Yesu, wakaingia katika muji mutakatifu Yerusalema, na watu wengi wakawaona. Mukubwa wa waaskari na wale waliokuwa pamoja naye wakimuchunga Yesu walipoona tetemeko la inchi na mambo yote yaliyofanyika, wakaogopa sana, na kusema: “Hakika mutu huyu alikuwa Mwana wa Mungu.” Pale kulikuwa vilevile wanawake wengi walioangalia kwa mbali; ndio wale waliomufuata Yesu tokea Galilaya, wakimushugulikia. Kati yao kulikuwa Maria wa Magdala, Maria mama ya Yakobo na Yosefu, pamoja na mama ya wana wa Zebedayo. Ilipokwisha kuwa magaribi, mutu mumoja tajiri aliyeitwa Yosefu wa Arimatea, akafika. Huyu naye alikuwa mwanafunzi wa Yesu. Yeye akaenda kwa liwali Pilato kwa kumwomba maiti ya Yesu. Basi Pilato akaamuru aipewe. Halafu Yosefu akatwaa maiti ile, akaifungafunga ndani ya vitambaa safi. Akaiweka ndani ya kaburi lake jipya alilojichimbia katika jiwe. Kisha akasukumia jiwe kubwa kwenye kiingilio cha lile kaburi na kujiendea. Maria wa Magdala na yule Maria mwingine walikuwa wakiikaa pale, kuelekea kwenye kaburi. Kesho yake, maana yake siku iliyofuata ile ya matayarisho ya siku ya Sabato, wakubwa wa makuhani na Wafarisayo wakamwendea Pilato, na kumwambia: “Bwana, tunakumbuka kwamba wakati yule mudanganyifu alipokuwa angali muzima, alisema: ‘Kwa siku tatu kisha kufa kwangu, nitafufuka.’ Basi uamuru kaburi lichungwe mpaka zile siku tatu nyuma ya kufa kwake zitakapotimia, kusudi wanafunzi wake wasifike kuiba maiti yake na kuwaambia watu kwamba amefufuka.” Pilato akawajibu: “Muko na waaskari walinzi. Muende kuchunga kaburi kwa kadiri munavyoweza.” Basi wakaenda, wakatia muhuri juu ya lile jiwe, na wakaweka waaskari pale kwa kulichunga. Siku ya Sabato ilipokwisha kupita, kesho yake siku ya kwanza ya juma, kwa wakati wa mapambazuko, Maria wa Magdala na Maria mwingine wakaenda kuangalia kaburi. Kwa rafla kukatokea tetemeko la inchi, kwa maana malaika wa Bwana alishuka toka mbinguni, akasukuma lile jiwe lililofunga kaburi pembeni na kuikaa juu yake. Yeye aliangaa kama umeme na nguo yake ilikuwa nyeupe sana. Halafu wale walinzi wa kaburi wakaogopa sana na kutetemeka, hata wakakuwa kama wamekufa. Yule malaika akawaambia wale wanawake: “Musiogope, kwa maana ninajua ya kama munamutafuta Yesu aliyetundikwa juu ya musalaba. Yeye hayuko hapa: amefufuka sawa alivyosema. Mukuje, muone pahali walipolalisha maiti yake. Muende upesi kuwaambia wanafunzi wake kwamba amefufuka, naye anawatangulia Galilaya, ni kule watakapomwona. Basi, nimekwisha kuwaambia ninyi.” Basi wale wanawake wakaondoka upesi kutoka kwenye kaburi, wakijazwa na woga na furaha kubwa vilevile. Wakakimbia kwenda kuwapasha wanafunzi wake habari ile. Mara moja Yesu akakutana na wale wanawake, akawasalimia. Wakajongea karibu naye, wakamushika miguu na kumwabudu. Kisha Yesu akawaambia: “Musiogope, muende kuwaambia wandugu zangu waende Galilaya, na kule wataniona.” Wale wanawake walipokuwa wakienda, waaskari wamoja kati ya wale waliochunga kaburi wakaenda katika muji na kuwapasha wakubwa wa makuhani habari za mambo yote yaliyotokea. Wakubwa wa makuhani wakakutana pamoja na wasimamizi wa watu na kukata shauri. Wakawapa wale waaskari feza nyingi wakiwaambia: “Mutasema kwamba wanafunzi wake walikuja kuiba maiti yake usiku wakati mulipokuwa mukilala usingizi. Na kama liwali akisikia habari hii, sisi tutasemezana naye na kuhakikisha yale yaliyotokea kusudi musipate matata.” Basi wale waaskari walinzi wakapokea zile feza na kufanya sawa walivyoambiwa. Na habari hii ilienea katikati ya Wayuda mpaka leo. Halafu wale wanafunzi kumi na mumoja wakaenda Galilaya kwa mulima ule Yesu aliowaagiza. Wakati walipomwona, wakamwabudu, lakini wamoja kati yao wakaona shaka. Kisha Yesu akakuja karibu nao, na kuwaambia: “Nimepewa mamlaka yote mbinguni na katika dunia. Basi muwaendee watu wa mataifa yote kusudi wapate kuwa wanafunzi wangu, mukiwabatiza kwa jina la Baba, la Mwana na la Roho Mutakatifu. Muwafundishe kutii maneno yote niliyowaagiza. Na mujue kwamba mimi ni pamoja nanyi siku zote hata mwisho wa dunia.” Huu ndio mwanzo wa Habari Njema ya Yesu Kristo, Mwana wa Mungu. Na imeandikwa hivi katika kitabu cha nabii Isaya: “Mungu anasema: ‘Ninamutuma mujumbe wangu akutangulie, kusudi akutengenezee njia.’ Sauti inatangaza katika jangwa: ‘Mutengeneze njia ya Bwana, munyooshe pahali atakapopita!’ ” Hivi Yoane alitokea katika jangwa, akibatiza watu, akiwahubiri kwamba wageuke toka zambi zao, wabatizwe, na Mungu atawasamehe. Watu wengi walitoka katika Yerusalema na katika jimbo lote la Yudea kwa kumwendea Yoane. Walikubali zambi zao, naye akawabatiza katika muto Yordani. Yoane alikuwa akivaa nguo iliyotengenezwa na manyoya ya ngamia na mukaba wa ngozi katika kiuno. Naye alikuwa akikula nzige na asali ya pori. Yeye alihubiri hivi kwa watu: “Yule anayekuja nyuma yangu ni mwenye uwezo kunipita; nami sistahili hata kuinama na kufungua kamba ya viatu vyake. Mimi nimewabatiza kwa maji, lakini yeye atawabatiza kwa Roho Mutakatifu.” Katika siku zile, Yesu akatoka Nazareti, katika Galilaya, akabatizwa na Yoane katika Yordani. Mara moja wakati Yesu alipotoka ndani ya maji, akaona mbingu zinafunguka na Roho Mutakatifu akishuka juu yake kwa mufano wa njiwa. Na sauti ikasikilika toka mbinguni, ikisema: “Wewe ndiwe Mwana wangu mupendwa; ninapendezwa nawe sana.” Kisha Roho Mutakatifu akamusukuma Yesu kwenda katika jangwa. Akabaki katika jangwa kwa muda wa siku makumi ine, na kule Shetani akamujaribu. Alikaa kule katikati ya nyama wa pori, nao wamalaika walimushugulikia. Nyuma ya kutiwa kwa Yoane katika kifungo, Yesu alikwenda Galilaya, akahubiri Habari Njema inayotoka kwa Mungu. Alisema: “Wakati umetimia, na Ufalme wa Mungu ni karibu! Mugeuke toka zambi zenu na kukubali Habari Njema!” Wakati Yesu alipokuwa akitembea pembeni ya ziwa la Galilaya akawaona wavuvi wawili, waliokuwa wandugu za tumbo: Simoni na ndugu yake Andrea. Walikuwa wakitupa nyavu katika ziwa lile. Yesu akawaambia: “Munifuate, nami nitawaweka kwa kazi ya kuopoa watu.” Mara moja wakaacha nyavu zao na kumufuata. Yesu alipoendelea mbele kidogo, akawaona wandugu wengine wawili: Yakobo na Yoane waliokuwa wana wa Zebedayo. Walikuwa ndani ya chombo wakitengeneza nyavu zao. Mara moja akawaita. Basi wakamwacha baba yao Zebedayo ndani ya chombo pamoja na watumishi wake, wakamufuata Yesu. Yesu na wanafunzi wake walienda Kapernaumu. Siku ya Sabato ilipotimia, Yesu akaingia katika nyumba ya kuabudia na kufundisha watu. Watu waliomusikia walishangaa sana kuona namna alivyofundisha, kwa maana hakuwafundisha sawa na walimu wao wa Sheria, lakini kama mutu mwenye mamlaka. Saa ile, mutu mumoja aliyeshikwa na pepo alikuwa ndani ya nyumba ya kuabudia. Akaanza kulalamika, akisema: “Kuna maneno gani kati yako na sisi, wewe Yesu wa Nazareti? Ulikuja kutuangamiza? Ninakutambua wewe ni nani: wewe ni Mutakatifu aliyetumwa na Mungu.” Yesu akamukaripia kwa nguvu, akimwamuru: “Nyamaza, na utoke ndani ya mutu huyu!” Yule pepo akamutikisa mutu yule kwa nguvu, akatoka ndani yake, akilalamika kwa nguvu. Watu wote wakashangaa sana na kuulizana: “Hatujaona mambo kama haya! Hakika mafundisho haya ni yenye mamlaka! Mutu huyu anaamuru hata pepo, nao wanamutii!” Halafu sifa za Yesu zikaenea upesi katika jimbo lote la Galilaya. Yesu na wanafunzi wake walipotoka ndani ya ile nyumba ya kuabudia, mara moja wakaenda kwa nyumba ya Simoni na Andrea, wakiwa pamoja na Yakobo na Yoane. Mama mukwe wa Simoni alikuwa katika kitanda, kwa sababu alikuwa na homa. Wakati Yesu alipofika pale, mara moja wakamupasha habari ya ugonjwa wake. Basi Yesu akajongea karibu naye, akamushika mukono na kumusimamisha. Naye akapona homa na kuanza kuwashugulikia. Ilipokuwa magaribi, jua lilipokuwa limekwisha kutua, wakamuletea Yesu watu wote waliokuwa wagonjwa na waliokuwa na pepo. Watu wote wa muji walikusanyika mbele ya mulango wa nyumba. Yesu akawaponyesha watu wengi wenye magonjwa mbalimbali. Vilevile alifukuza pepo wengi, wala hakuwaachilia pepo kusema neno, kwa sababu walimujua yeye ni nani. Kesho yake asubui kulipokuwa kungali giza, Yesu akaamuka, akatoka katika muji na kwenda pahali penye ukiwa, kule akaanza kuomba. Basi Simoni na wenzake wakaenda kumutafuta. Nao walipomwona wakamwambia: “Watu wote wanakutafuta.” Lakini Yesu akawajibu: “Twende pahali pengine katika vijiji vinavyokuwa karibu, kusudi nihubiri kule vilevile, kwa maana ni kwa ajili ya ile nimekuja.” Hivi akaenda fasi zote katika Galilaya, akihubiri katika nyumba za kuabudia na kufukuza pepo. Mutu mumoja mwenye ukoma alikuja kwa Yesu, akapiga magoti mbele yake na kumusihi, akisema: “Kama ukitaka, unaweza kunitakasa.” Yesu akamusikilia huruma, akanyoosha mukono, akamugusa na kumwambia: “Ninataka utakaswe!” Na mara moja mutu yule akapona ukoma na kutakaswa. Pale pale Yesu akamwagiza kwa nguvu aende na kusema: “Angalisho, usimwambie mutu hata neno moja juu ya hii. Lakini kwenda kwa kuhani na kumwonyesha jinsi unavyokuwa sasa. Kisha utoe sadaka kama Musa alivyoamuru, kuwa ushuhuda kwa wote kwamba umetakaswa.” Lakini mutu yule alipoenda, akaanza kutangaza habari zile fasi zote. Na kwa sababu hii Yesu hakuweza kuingia tena waziwazi katika muji wowote, lakini alibaki mbali nayo pahali penye ukiwa. Na watu walimufikia kule kutoka pande zote. Nyuma ya siku chache, Yesu akarudi Kapernaumu, na watu wakasikia kwamba yuko ndani ya nyumba. Watu wengi wakakusanyika pale mpaka hapakukuwa tena nafasi ndani ya nyumba, hata inje mbele ya mulango. Yesu alipokuwa akiwahubiri Neno la Mungu, wakamuletea mugonjwa mwenye kupooza, akibebwa na watu wane. Lakini kwa kuona hawakuweza kumufikisha mbele ya Yesu kwa sababu ya uwingi wa watu, wakabomoa dari juu ya pahali Yesu alipokuwa. Kisha wakamushusha yule mwenye kupooza kwenye nafasi ile walipobomoa, akilala juu ya kipoyi chake. Yesu alipoona namna walivyomwaminia, akamwambia yule mwenye kupooza: “Mutoto wangu, zambi zako zimesamehewa.” Walimu wamoja wa Sheria walioikaa pale wakajiuliza: “Namna gani mutu huyu anasubutu kumutukana Mungu? Ni nani anayeweza kusamehe zambi isipokuwa Mungu peke yake?” Mara moja Yesu akitambua mafikiri yao, akawauliza: “Sababu gani munajiuliza mambo hayo yote? Kitu gani kinachokuwa chepesi: kumwambia mutu mwenye kupooza ‘Zambi zako zimesamehewa’ au kumwambia ‘Simama, utwae kipoyi chako na utembee?’ Basi, ninataka mujue kwamba Mwana wa Mutu yuko na mamlaka ya kusamehe zambi hapa katika dunia.” Kwa hiyo akamwambia yule mutu mwenye kupooza: “Ninakuamuru, simama, utwae kipoyi chako na uende kwako!” Na watu wote walipokuwa wakimwangalia mutu yule, pale pale akasimama, akatwaa kipoyi chake na kujiendea. Wote wakashangaa, wakamusifu Mungu, wakisema: “Hatujaona mambo kama haya hata mara moja!” Yesu akaenda tena pembeni ya ziwa la Galilaya. Kundi kubwa la watu wakamufikia, naye akawafundisha. Kisha alipokuwa akipita, akamwona Lawi mwana wa Alfayo, akiikaa katika nyumba ya kulipishia kodi. Yesu akamwambia: “Unifuate!” Naye Lawi akasimama na kumufuata. Nyuma Yesu akaikaa kula chakula ndani ya nyumba ya Lawi. Walipishaji wengi wa kodi na watenda mabaya wengine waliikaa kula pamoja na Yesu na wanafunzi wake, kwa maana watu wengi wa namna ile walikuwa wamemufuata. Na wakati walimu wa Sheria wa kikundi cha Wafarisayo walipomwona Yesu akikula pamoja na watu wale, wakawauliza wanafunzi wake: “Kwa sababu gani anakula pamoja na walipishaji wa kodi na watenda mabaya?” Yesu alisikia vile walivyosema, na kwa hiyo akawaambia: “Wenye afya nzuri hawahitaji muganga, ni wale wanaokuwa wagonjwa tu. Sikukuja kuwaita wenye haki kunifuata, lakini watenda mabaya.” Wanafunzi wa Yoane Mubatizaji na Wafarisayo walikuwa wakifunga kula chakula. Hivi watu wakakuja kumwuliza Yesu: “Sababu gani wanafunzi wa Yoane Mubatizaji na wanafunzi wa Wafarisayo wanafunga kula chakula, lakini wanafunzi wako hawafungi?” Yesu akawajibu: “Munafikiri kwamba wanaoalikwa kwa arusi wanaweza kujizuiza kula chakula cha karamu wakati bwana-arusi angali pamoja nao? Hapana! Wakati bwana-arusi angali pamoja nao hawawezi kujizuiza kula. Lakini kutakuwa siku bwana-arusi atakapoondoshwa kati yao; ni katika siku zile ndipo watafunga kula. “Hakuna mutu anayeshonea kiraka kipya juu ya nguo ya zamani. Kama akifanya vile, kile kiraka kipya kinapasua nguo ya zamani, nako kupasuka kwake kunaongezeka zaidi. Vilevile hakuna mutu anayetia divai mupya ndani ya machupa ya ngozi yenye kuzeeka. Kama akifanya vile, ile divai mupya itapasua machupa yale yenye kuzeeka, nayo divai na machupa vyote vinapotea bure. Lakini inafaa kutia divai mupya ndani ya machupa mapya ya ngozi.” Siku moja ya Sabato Yesu akapita katika mashamba ya ngano. Wanafunzi wake wakaanza kuchumachuma masuke ya ngano kwa kadiri walivyoendelea katika njia. Basi Wafarisayo wakamwambia Yesu: “Sababu gani wanafunzi wako wanafanya jambo linalokatazwa kwa siku ya Sabato?” Yesu akawajibu: “Hamujasoma bado vile Daudi alivyofanya wakati alipohitaji chakula, kwa sababu yeye mwenyewe na watu wake walisikia njaa? Si aliingia ndani ya nyumba ya Mungu na kula mikate mitakatifu iliyotolewa kwa Mungu? Jambo hili lilifanyika wakati Abiatari alipokuwa Kuhani Mukubwa. Ni makuhani tu walioruhusiwa kula mikate ile, lakini Daudi alikula na kuwapa watu wake vilevile.” Yesu akaongeza kuwaambia: “Siku ya Sabato iliwekwa kwa ajili ya mafaa ya mutu, lakini mutu hakuumbwa kwa ajili ya siku ya Sabato. Ni kwa sababu hii, Mwana wa Mutu ndiye Bwana hata wa siku ya Sabato.” Yesu aliingia tena katika nyumba ya kuabudia. Na mule ndani mulikuwa mutu mumoja mwenye mukono unaokauka. Watu waliokuwa mule wakamuchunguza Yesu kusudi waone kama atamuponyesha mutu yule kwa siku ya Sabato, wapate sababu ya kumushitaki. Halafu Yesu akamwambia yule mwenye mukono unaokauka: “Simama hapa katikati.” Kisha akawauliza: “Sheria inaturuhusu kufanya mema au kufanya mabaya kwa siku ya Sabato? Kuponyesha mutu au kumwua?” Lakini wakakaa kimya. Yesu akawakazia macho kwa kasirani, akihuzunika kwa sababu ya ugumu wao. Akamwambia yule mutu: “Nyoosha mukono wako.” Akaunyoosha, nao ukakuwa muzima tena. Pale pale Wafarisayo wakatoka inje na kwenda kukusanyika na watu wa Herode kusudi wafanye mipango ya kumwua Yesu. Yesu na wanafunzi wake wakaenda peke yao pembeni ya ziwa la Galilaya, na kundi kubwa la watu walimufuata. Watu hawa walitoka Galilaya na Yudea, Yerusalema, Idumea, katika inchi za upande mwengine wa muto Yordani na pande za muji wa Tiro na wa Sidona. Kundi hili kubwa la watu walimufikia Yesu kwa sababu walisikia habari za mambo aliyofanya. Na kwa kuona uwingi wa watu wale, Yesu akawaambia wanafunzi wake wamutayarishie chombo kidogo kusudi wasimusonge. Watu waliokuwa na magonjwa walikuwa wakisukumana kusudi wamufikie na kumugusa kwa maana aliwaponyesha watu wengi. Na wakati pepo walipomwona Yesu, wakaanguka mbele yake na kulalamika, wakisema: “Wewe ni Mwana wa Mungu.” Lakini Yesu aliwakaripia kwa nguvu wasimutambulishe yeye ni nani. Kisha Yesu akapanda juu ya kilima, akawaita watu aliowataka mwenyewe, nao wakakuja kwake. Akachagua kumi na wawili kati yao, kusudi wakae pamoja naye na apate kuwatuma kwa kuhubiri, na kuwapa uwezo wa kufukuza pepo. Wale kumi na wawili aliowachagua ni hawa: Simoni (Yesu aliyemupa jina la Petro), Yakobo na ndugu yake Yoane, wote wawili walikuwa wana wa Zebedayo (Yesu aliwapa jina la Boanerge, maana yake ngurumo ya radi), Andrea na Filipo, Bartolomayo, Matayo, Toma, Yakobo mwana wa Alfayo, Tadeo, Simoni wa kundi la Wazeloti na Yuda Iskariota, yule aliyemutoa Yesu. Kisha Yesu akarudi kwenye nyumba. Kundi kubwa la watu wakakusanyika tena hata Yesu na wanafunzi wake hawakupata wakati wa kula. Wandugu zake za jamaa waliposikia maneno haya, wakaondoka kwenda kumutwaa, kwa maana walisema kwamba amepotelewa na akili. Walimu wa Sheria waliotoka Yerusalema, wakasema hivi juu ya Yesu: “Amepatwa na Belzebuli.” Na wengine wao wakasema: “Ni huyo mukubwa wa pepo ndiye anayemupa uwezo wa kufukuza pepo.” Basi Yesu akawaita, akawaambia kwa mifano akisema: “Namna gani Shetani anaweza kujifukuza mwenyewe? Watu wa ufalme mumoja wakigombana wao kwa wao, ufalme ule utaanguka. Nao watu wa jamaa moja wakigombana wao kwa wao, jamaa ile haitadumu. Kama Shetani akijigombanisha yeye mwenyewe, na ufalme wake ukigawanyika, uwezo wake hautaendelea, lakini utaanguka. “Mutu hawezi kuingia ndani ya nyumba ya mwenye nguvu na kunyanganya vitu vyake, isipokuwa kwanza anamufunga. Kisha anaweza kunyanganya vitu vyake. “Kweli ninawaambia: watu wataweza kusamehewa zambi zao zote na matusi yao yote. Lakini mutu anayemutukana Roho Mutakatifu hatasamehewa hata milele, kwa maana zambi ile inadumu kwa milele.” Yesu aliwaambia vile kwa sababu walisema kwamba yuko na pepo. Mama ya Yesu na wandugu zake wakakuja, wakasimama inje, wakatuma mutu kwenda kumwita. Kundi kubwa la watu waliikaa, wakizunguka Yesu. Halafu wakamwambia: “Mama yako na wandugu zako wako inje, wanakutafuta.” Yesu akawajibu: “Nani ndiye mama yangu, na nani ndio wandugu zangu?” Kisha akawaangalia watu waliomuzunguka, na kusema: “Mama yangu na wandugu zangu, ni hawa wanaoikaa hapa. Kwa sababu mutu yeyote anayefanya mapenzi ya Mungu, huyu ndiye ndugu yangu, dada yangu na mama yangu.” Yesu alianza kufundisha tena pembeni ya ziwa la Galilaya. Kundi kubwa la watu walikusanyika karibu naye, kwa hiyo akaingia ndani ya chombo na kuikaa mule. Chombo kilikuwa katika ziwa na watu walisimama inchi kavu, pembeni ya ziwa. Yesu akawafundisha mambo mengi akitumia mifano. Yeye akawaambia hivi katika mafundisho yake: “Musikilize! Mutu mumoja alikwenda kupanda mbegu. Alipokuwa akipanda mbegu katika shamba, zimoja zikaanguka pembeni ya njia, nao ndege wakakuja na kuzikula. Zingine zikaanguka pahali penye mawe pasipokuwa udongo mwingi. Mbegu zile zikaota upesi kwa sababu hapakukuwa udongo mwingi. Wakati jua lilipokuwa kali, likazichoma, na kwa sababu hazikukuwa na mizizi mikubwa zikakauka. Mbegu zingine zilianguka katikati ya miiba. Ile miiba ikaota na kuzisonga mbegu hata hazikuweza kutoa kitu. Lakini mbegu zingine zikaanguka katika udongo muzuri, mimea ikaota, ikakomaa na kuzaa matunda: zimoja zikazaa punje makumi tatu, zingine makumi sita na zingine punje mia moja.” Kisha akawaambia: “Mwenye kuwa na masikio ya kusikia, asikie!” Wanafunzi kumi na wawili wa Yesu pamoja na watu waliokuwa pembeni yake walipokuwa peke yao, wakamwuliza awaelezee maana ya mifano ile. Yesu akawajibu: “Ninyi mumefunuliwa kujua siri ya Ufalme wa Mungu, lakini watu wengine wanaokuwa inje ya kikundi chenu wanasikia mambo yote kwa njia ya mifano, kusudi ‘Wapate kuangalia, lakini wasione; nao wapate kusikia, lakini wasikuwe na ufahamu, kusudi wasipate kumugeukia Mungu na kusamehewa.’ ” Yesu akaongeza kuwaambia: “Kama musipoelewa mufano huu, namna gani mutaelewa mifano mingine? Mupandaji anapanda Neno la Mungu. Nafasi ile mbegu zilipoanguka pembeni ya njia, ni mufano wa watu wanaosikia Neno la Mungu, lakini mara moja Shetani anakuja na kuondoa lile Neno lililopandwa ndani yao. Udongo wenye mawe, pahali mbegu zilipoanguka ni mufano wa watu wanaosikia Neno la Mungu, na mara moja wanalipokea kwa furaha. Lakini halizami ndani yao kama mizizi; wanalishika kwa muda mufupi tu. Wakati taabu na mateso vinapowafikia kwa ajili ya Neno la Mungu, mara moja wanaanguka. Udongo wenye miiba, pahali mbegu zilipoanguka, ni mufano wa wale wanaosikia Neno la Mungu, lakini masumbuko ya dunia hii, udanganyifu wa mali, na tamaa za namna nyingine vikiwaingia, vinasonga lile Neno linalokuwa ndani yao na kulizuiza kuzaa matunda. Nao udongo muzuri, walimopanda mbegu, ni mufano wa watu wanaosikia Neno la Mungu na kulipokea. Nao wanazaa matunda; wamoja matunda makumi tatu, wengine makumi sita na wengine mia moja.” Kisha Yesu akawaambia: “Taa inaletwa kwa kufunikiwa chini ya kitunga au chini ya kitanda? Si wanaiweka juu ya kinara? Ni hivi vilevile hakuna chochote kinachofichwa kitakachokosa kuonekana wazi, wala hakuna siri itakayokosa kufunuliwa waziwazi. Mwenye kuwa na masikio ya kusikia, asikie!” Yesu akawaambia tena: “Muangalie vizuri maneno munayosikia! Mungu atawapimia na kipimo kile munachowapimia wengine, na kuwaongezea hata zaidi. Kwa maana anayekuwa na kitu, ataongezewa kingine; lakini asiyekuwa na kitu, ataondolewa hata kidogo anachokuwa nacho.” Yesu akaendelea kusema: “Ufalme wa Mungu unafanana na mutu mumoja aliyepanda mbegu katika shamba lake. Kila siku alilala na kuamuka na mbegu ziliota na kukomaa. Lakini hakujua namna gani mbegu zilivyoota. Udongo wenyewe unaotesha mimea; kwanza majani, halafu masuke na kisha ngano zinazokomaa ndani ya masuke. Wakati ngano zinapokomaa, mutu anazivuna, kwa maana ni wakati wa mavuno.” Yesu akasema tena: “Tufananishe Ufalme wa Mungu na nini? Au tuulinganishe na mufano gani? Unafanana na mbegu ya haradali. Inapopandwa katika udongo ni ndogo sana kuliko mbegu zote za dunia. Lakini ikiisha kupandwa, inaota na kuwa kubwa zaidi kuliko mimea yote. Inatoa matawi makubwa hata ndege wanaweza kujenga chicha zao juu yake, kwenye kivuli chake.” Yesu aliwafundisha watu kwa mifano mingi ya namna hii kwa kadiri walivyoweza kuelewa. Hakusema nao pasipo kutumia mifano lakini alipokuwa pamoja na wanafunzi wake peke yao, aliwafasiria mambo yote. Na ilipotimia magaribi siku ile ile, Yesu akawaambia wanafunzi wake: “Tuvuke ngambo ingine ya ziwa.” Basi wanafunzi wakaaga kundi la watu, wakaingia ndani ya chombo Yesu alimokuwa na kuondoka pamoja naye. Na vyombo vingine vikamusindikiza. Zoruba kali ikavuma ndani ya ziwa, maji yakajitupatupa ndani ya chombo hata kikaanza kujaa. Yesu alikuwa upande wa nyuma wa chombo, akilala usingizi akilalisha kichwa juu ya mufuko wa kuegemea. Wanafunzi wake wakamwamusha na kumwambia: “Mwalimu, haikuhangaishi kuona sisi tunakufa?” Yesu akaamuka, akakaripia ile zoruba na kuiambia ziwa: “Kimya! Tulizana!” Basi zoruba ikakoma na kukakuwa kimya kabisa. Kisha Yesu akawaambia wanafunzi: “Sababu gani munaogopa? Mpaka sasa hamujakuwa na imani?” Halafu wakaogopa sana, nao wakaanza kuulizana: “Huyu ni mutu gani, hata zoruba na ziwa vinamutii?” Kisha Yesu na wanafunzi wake wakafika kule ngambo ingine ya ziwa la Galilaya katika inchi ya Wagerasi. Yesu alipotoka ndani ya chombo, pale pale mutu mumoja aliyeshikwa na pepo akakuja kukutana naye akitoka kwenye makaburi. Makao ya mutu huyu yalikuwa katika makaburi, wala hakuna mutu aliyeweza kumufunga tena hata na minyororo. Mara nyingi miguu yake ilifungwa vifungo vya chuma, nayo mikono yake na minyororo, lakini alikata minyororo ile na kuvunjavunja vile vifungo vya chuma. Hakuna mutu aliyekuwa na nguvu ya kumushinda. Saa zote, usiku na muchana alitangatanga katikati ya makaburi na kwenye milima, akilalamika na kujiumizaumiza kwa mawe. Alipomwona Yesu kwa mbali, akaenda mbio na kumupigia magoti na kulalamika kwa nguvu, akisema: “Yesu, Mwana wa Mungu Mukubwa, kuna neno kati yako na mimi? Ninakusihi kwa jina la Mungu, usinitese!” (Alisema hivi kwa sababu Yesu alikuwa akimwamuru: “Wewe pepo, toka ndani ya mutu huyu!”) Basi Yesu akamwuliza: “Jina lako nani?” Naye akamujibu: “Jina langu ni ‘Jeshi’, maana sisi ni wengi.” Akazidi kumusihi Yesu kwamba asiwatoshe wale pepo katika inchi ile. Na pale karibu na mulima kulikuwa kundi kubwa la nguruwe wakijitafutia chakula. Basi pepo wakamusihi Yesu kwamba awatume kuingia ndani ya nguruwe wale. Yesu akawaruhusu. Halafu wale pepo wakatoka ndani ya mutu yule na kuingia ndani ya nguruwe. Kundi zima la nguruwe, karibu elfu mbili, wakatelemuka mbio kwenye mulima na kutumbukia ndani ya ziwa, nao wakazama ndani ya maji. Wachungaji wa nguruwe wakaenda mbio kupasha habari katika muji na katika vijiji. Watu wakakuja kusudi waone jambo lililotokea. Walipomufikia Yesu, wakamwona yule aliyekuwa na kundi la pepo ndani yake akiikaa, akiwa amevaa nguo nayo akili yake ikiwa sawa. Basi watu wale wakaogopa. Nao walioona yale yaliyotendeka wakawaelezea watu wale mambo yaliyomutokea yule aliyekuwa na pepo na yaliyotokea nguruwe. Kwa hiyo wakaanza kumusihi Yesu aondoke katika inchi yao. Yesu alipokuwa akiingia katika chombo, yule aliyekuwa na pepo akamusihi aende pamoja naye. Yesu hakumuruhusu, lakini akamwambia: “Kwenda kwako kwenye jamaa yako, na uwaelezee mambo Bwana aliyokutendea na namna alivyokuhurumia.” Basi yule mutu akajiendea, akaanza kutangaza mambo yote Yesu aliyomutendea katika inchi ya Miji Kumi. Na watu wote waliomusikia wakashangaa sana. Yesu akavuka ngambo ingine ya ziwa la Galilaya. Alipokuwa pembeni ya ziwa, watu wengi wakakusanyika karibu naye. Halafu mukubwa mumoja wa nyumba ya kuabudia aliyeitwa Yairo, akafika pale. Alipomwona Yesu, akajitupa mbele yake, akamusihi sana, akisema: “Binti yangu mudogo yuko karibu kufa. Ninakuomba ukuje kwanza kwa kuweka mikono yako juu yake, kusudi apate kupona na kuishi!” Basi Yesu akaenda pamoja naye. Watu wengi walimufuata na kumusongasonga. Na kati yao kulikuwa mwanamuke mumoja mwenye ugonjwa wa kutokwa na damu kwa muda wa miaka kumi na miwili. Aliwaendea waganga wengi, lakini ingawa vile aliteswa sana na kupoteza mali yake. Yeye hakuweza kupona, lakini hali yake iliendelea kuwa mbaya zaidi. Wakati mwanamuke yule aliposikia habari za Yesu, alikuja na kuingia katikati ya kundi la watu nyuma ya Yesu na kugusa nguo yake, kwa sababu alikuwa akijisemesha: “Kama nikiweza tu kugusa nguo ya Yesu nitapona.” Alipogusa nguo ya Yesu, mara moja damu yake ikaacha kutoka, naye akajisikia amepona. Na mara moja Yesu akatambua kama nguvu zilitoka ndani yake. Basi akageuka kati ya kundi na kuuliza: “Ni nani aliyegusa nguo yangu?” Wanafunzi wake wakamujibu: “Hauoni namna watu wanavyokusongasonga? Namna gani unauliza kwamba ni nani aliyekugusa?” Lakini Yesu akaangalia pande zake zote kusudi amwone yule aliyefanya vile. Yule mwanamuke akaogopa na kuanza kutetemeka, kwa sababu alitambua yote yaliyomutukia. Halafu akakuja kujitupa kwa miguu yake na kumwambia ukweli wote. Yesu akamwambia: “Binti yangu, imani yako imekuponyesha. Ujiendee na amani, ugonjwa wako umepona!” Yesu alipokuwa hajamaliza kusema maneno haya, wajumbe wakafika kutoka kwa yule mukubwa wa nyumba ya kuabudia na kumwambia: “Binti yako amekwisha kufa. Basi kwa sababu gani ungali unamusumbua Mwalimu?” Lakini Yesu hakuangalia maneno yao, akamwambia yule mukubwa: “Usiogope, uamini tu.” Na Yesu hakuruhusu mutu kumusindikiza, isipokuwa Petro, Yakobo, na Yoane, yule ndugu wa tumbo wa Yakobo. Walipofika kwa nyumba ya mukubwa Yairo, Yesu akakuta kuko makelele, nao watu wakilia na kulalamika sana. Akaingia ndani ya nyumba, akawaambia: “Kwa nini munafanya makelele na kulia? Mutoto hakukufa, lakini analala tu!” Nao wakaanza kumuchekelea. Halafu Yesu akawaondosha wote inje, akawakamata wazazi wa yule mutoto na wanafunzi wake watatu, akaingia katika chumba pahali mutoto alipokuwa. Akashika mukono wa mutoto, akamwambia: “Talita kumu,” maana yake: “Kijana binti, ninakuambia, amuka!” Mara moja yule kijana akasimama na kuanza kutembea (alikuwa na umri wa miaka kumi na miwili). Nao watu wakashangaa sana kwa kuona jambo hilo. Lakini Yesu aliwaagiza sana wasimwambie mutu yeyote jambo lililofanyika. Kisha akawaambia wamupe mutoto yule chakula. Yesu akatoka kule, akaenda katika muji wake wa kuzaliwa, nao wanafunzi wake wakamufuata. Siku ya Sabato ilipotimia, akaanza kufundisha katika nyumba ya kuabudia. Watu wengi waliomusikiliza, wakashangaa sana na kuulizana: “Huyu amepata maneno haya yote kutoka wapi? Ni hekima ya namna gani aliyopata? Ni kwa uwezo wa namna gani anafanya miujiza kama hii? Huyu si yule museremala, mwana wa Maria, ndugu ya Yakobo, Yose, Yuda na Simoni? Nao wadada zake, si wanaishi hapa kati yetu?” Na kwa hiyo wakakosa kumwaminia. Lakini Yesu akawaambia: “Nabii hakosewi heshima fasi zote, isipokuwa tu katika muji wake, katikati ya wandugu zake na katika jamaa yake.” Kwa hiyo Yesu hakuweza kufanya muujiza wowote kule, isipokuwa aliweka mikono yake juu ya wagonjwa wachache na kuwaponyesha. Naye alishangaa sana kwa sababu ya kutokuamini kwa watu wale. Kisha Yesu akazunguka katika vijiji vya kandokando akiwafundisha watu. Aliwaita wanafunzi wake kumi na wawili, akaanza kuwatuma wawili wawili na kuwapatia uwezo wa kufukuza pepo. Akawaagiza: “Musibebe kitu chochote kwa safari yenu isipokuwa fimbo tu. Musibebe chakula, mufuko, wala feza ndani ya mikaba yenu. Muvae viatu lakini musivae kanzu mbili.” Akawaambia tena: “Nafasi yoyote watakapowakaribisha ndani ya nyumba, mubakie mule mpaka mutakapotoka kule. Na nafasi yoyote watu watakapokataa kuwakaribisha na kuwasikiliza, mutoke kule na mukungute mavumbi toka juu ya miguu yenu. Jambo hili litakuwa ushuhuda juu yao.” Basi wanafunzi wakaondoka, wakahubiri watu kwamba wageuke toka zambi zao. Wakafukuza pepo wengi, na wakapakaa wagonjwa wengi mafuta na kuwaponyesha. Mufalme Herode alisikia habari za Yesu, kwa maana jina lake lilikuwa limevuma fasi zote. Watu wamoja walisema: “Huyu ni Yoane Mubatizaji aliyefufuka! Ni kwa sababu hii amepata uwezo wa kufanya miujiza.” Lakini wengine walisema: “Huyu ni nabii Elia.” Wengine walisema: “Yeye ni nabii sawa na mumoja wa wale manabii wa zamani.” Lakini Herode aliposikia habari zile, akasema: “Ni yule Yoane Mubatizaji niliyemukata kichwa ndiye amefufuka!” Ni Herode mwenyewe aliyeamuru kwamba Yoane akamatwe na kutiwa katika kifungo. Ilitokea vile kwa sababu Herode alimwoa Herodia, muke wa ndugu yake Filipo. Yoane alikuwa amemwambia kwamba hana sheria ya kumwoa yule muke wa mudogo wake. Kwa hiyo Herodia akamuwekea Yoane chuki na kutaka kumwua, lakini hakuweza kwa sababu ya Herode. Herode alimwogopa Yoane, kwa sababu alijua kwamba Yoane ni mwenye haki na mutakatifu. Kwa hivi alimulinda. Alipenda kumusikiliza, ijapokuwa alifazaika sana kila mara alipomusikia. Siku moja Herodia alipata wakati wa kumwua Yoane. Ilikuwa sikukuu ya kuzaliwa kwa Herode, wakati alipofanya karamu kwa wasimamizi wa serikali yake, wakubwa wa waaskari na waheshimiwa wa Galilaya. Binti ya Herodia aliingia na kucheza hata Herode na waalikwa wake wakapendezwa. Halafu mufalme akamwambia yule binti: “Uniombe kitu chochote unachotaka, nami nitakupa.” Kisha akamwapia, akisema: “Nitakupa chochote utakachoniomba, hata ikiwa nusu ya ufalme wangu.” Basi yule binti akatoka na kwenda kumwuliza mama yake: “Niombe nini?” Mama yake akamujibu: “Omba kichwa cha Yoane Mubatizaji.” Mara moja yule binti akarudi upesi kwa mufalme na kumwomba: “Ninataka unipe sasa hivi kichwa cha Yoane Mubatizaji katika sahani.” Mufalme akahuzunika sana, lakini hakumukatalia kwa sababu ya viapo alivyovitoa na kwa sababu ya waalikwa wake. Mara moja mufalme akamutuma mumoja wa waaskari wake walinzi na kumwamuru aende kuleta kichwa cha Yoane Mubatizaji. Yule askari akaenda ndani ya kifungo na kumukata Yoane kichwa. Kisha akakileta katika sahani, akamupa yule binti, naye akakipatia mama yake. Wakati wanafunzi wa Yoane walipopata habari ile, wakaenda kubeba maiti yake na kuizika. Mitume wakarudi kwa Yesu, na kumwelezea mambo yote waliyofanya na yote waliyofundisha. Watu waliomufikia Yesu na kuondoka walikuwa wengi sana hata yeye na wanafunzi wake hawakupata wakati wa kula. Kwa sababu hii aliwaambia wanafunzi: “Twende peke yetu kwa pahali penye ukiwa kusudi mupumzike kidogo.” Basi wakaenda peke yao ndani ya chombo kwa pahali penye ukiwa. Lakini watu wengi waliwaona wakiondoka, wakawatambua. Kwa hiyo wakaenda kule mbio kwa miguu toka miji yote, wakawatangulia kule walipokuwa wakienda. Wakati Yesu alipotoka ndani ya chombo, akaona kundi kubwa la watu, akawasikilia huruma, kwa sababu walikuwa kama kondoo wasiokuwa na muchungaji. Basi akaanza kuwafundisha maneno mengi. Ilipofika saa za magaribi, wanafunzi wa Yesu wakamufikia na kumwambia: “Hapa ni pori na sasa ni magaribi. Uwaage watu hawa kusudi waende kwenye nyumba kule katika mbuga na katika vijiji vya hapa karibu wapate kujinunulia chakula.” Yesu akawajibu: “Ninyi wenyewe muwape chakula.” Lakini wakamwuliza: “Unataka tuende kununua mikate kwa bei ya vikoroti mia mbili vya feza?” Naye Yesu akawauliza: “Muko na mikate ngapi? Muende kwanza kuangalia.” Walipokwisha kujua, wakamwambia: “Tuko na mikate mitano na samaki mbili.” Basi Yesu akawaamuru wanafunzi wake wawaambie watu wote waikae chini kwenye majani kwa makundi mbalimbali. Wakaikaa kwa makundi ya watu mia moja mia moja, na makumi tano tano. Kisha Yesu akatwaa ile mikate mitano na samaki mbili, akainua macho mbinguni, akamushukuru Mungu. Akamega ile mikate, akawapa wanafunzi wake pamoja na zile samaki mbili kusudi waigawanyie watu wote. Wote wakakula na kushiba. Kisha wanafunzi wakaokota vipande vya mikate na vya samaki vilivyobaki, wakajaza vitunga kumi na viwili. Hesabu ya wanaume tu waliokula ilikuwa elfu tano. Pale pale Yesu akawalazimisha wanafunzi wake waingie ndani ya chombo na kumutangulia ngambo ingine ya ziwa la Galilaya kuelekea muji Betesaida. Kwa wakati ule alibaki akiaga lile kundi la watu. Kisha kuwaaga, akaenda kwenye kilima kwa kuomba. Giza lilipoingia, chombo kilikuwa katikati ya ziwa, na Yesu alikuwa peke yake inchi kavu. Aliwaona wanafunzi wake wakitaabika kwa kuendesha chombo sababu upepo ulikuwa ukiwarudisha nyuma. Basi ilipokuwa karibu na mapambazuko, Yesu akawafikia akitembea juu ya maji, akitaka kuwapita. Nao walipomwona akitembea juu ya maji, wakawaza kwamba ni muzimu, wakaanza kulalamika, kwa maana wote walimwona na kuogopa sana. Lakini mara moja Yesu akasema nao na kuwaambia: “Mujipe moyo, ni mimi! Musiogope!” Kisha akaingia ndani ya chombo walimokuwa, na upepo ukakoma. Kwa hiyo wanafunzi wakashangaa sana, kwa maana hawakuelewa maana ya ule muujiza wa kuzidisha mikate; kwa kuwa mioyo yao ilikuwa migumu. Walipovuka ziwa, wakafika katika inchi ya Genezareti, wakaezeka chombo kwenye kivuko. Walipotoka ndani ya chombo, mara moja watu wakamutambua Yesu. Basi wakaenda mbio wakipita katika inchi ile yote, wakaanza kumuletea wagonjwa wakibebwa juu ya vipoyi, wakamufikia Yesu popote waliposikia yuko. Na kila pahali Yesu alipokwenda, katika vijiji, miji, au kwenye mbuga, watu waliweka wagonjwa katika viwanja vya makutano na kumusihi awaache wagonjwa waguse hata upindo wa kanzu yake tu. Nao wote waliougusa, walipona. Wafarisayo na walimu wamoja wa Sheria waliotoka Yerusalema wakakusanyika mbele ya Yesu. Wakawaona wanafunzi wake wamoja wakikula chakula na mikono michafu, maana yake, mikono waliyokosa kunawa kufuatana na desturi ya dini yao. Ilikuwa vile kwa maana Wafarisayo na Wayuda wote wanashika desturi za babu zao; zinazokataza kula pasipo kunawa mikono kama inavyostahili. Tena, wanapotoka kwa soko, hawakuli pasipo kuoga kwanza. Na zaidi ya hii wanashika desturi zingine nyingi kama vile namna ya kusafisha vikombe, mitungi na vyungu vilivyotengenezwa na shaba. Basi Wafarisayo na walimu wa Sheria wakamwuliza Yesu: “Sababu gani wanafunzi wako hawafuati desturi za babu zetu, lakini wanakula chakula na mikono michafu?” Yesu akawajibu: “Isaya alitabiri vema wakati alipoandika maneno haya juu yenu ninyi wanafiki: ‘Mungu anasema: Watu hawa wananiheshimu kwa midomo yao, lakini mioyo yao ni mbali nami. Ibada wanayonifanyia ni ya bure, sababu mafundisho yao yanalingana na kanuni za watu tu.’ ” Yesu akaendelea kuwaambia: “Munaacha amri za Mungu pembeni na kushika desturi za watu. Munajua vizuri namna ya kutupilia amri za Mungu kusudi mushike desturi zenu! Maana Musa alisema: ‘Uwaheshimu baba yako na mama yako,’ na, ‘Anayemutukana baba yake au mama yake, anapaswa kuuawa.’ Lakini ninyi munasema kwamba mutu akiwa na kitu cha kumusaidia baba au mama yake, lakini akimwambia kwamba kitu kile ni Korbane, (maana yake, kimetolewa kuwa sadaka takatifu kwa Mungu), munamuruhusu asiwasaidie wazazi wake. Hivi munazarau Neno la Mungu kwa ajili ya desturi zenu munazopokezana. Nanyi munafanya mambo mengine mengi ya namna ile.” Kisha Yesu akaita tena kundi la watu na kuwaambia: “Ninyi wote munisikilize na kuelewa maneno haya. Hakuna kitu kinachoingia ndani ya mutu kutoka inje kinachoweza kumuchafua. Lakini kitu kinachotoka ndani yake ndicho kinachomuchafua. [ Mwenye kuwa na masikio ya kusikia, asikie.]” Wakati Yesu alipoachana na kundi na kuingia ndani ya nyumba, wanafunzi wake wakamwuliza maana ya mufano ule. Naye akawaambia: “Hata ninyi vilevile hamuwezi kuelewa? Hamufahamu kwamba kila kitu kinachoingia ndani ya mutu kutoka inje hakiwezi kumuchafua? Kitu kile hakiingii ndani ya moyo wake, lakini kinaingia tu ndani ya tumbo na kisha kinatoka na kwenda katika choo.” (Kwa kusema hivi Yesu alionyesha kwamba vyakula vyote vinaruhusiwa kukuliwa.) Yesu akaongeza kusema: “Ni kile kinachotoka ndani ya mutu ndicho kinachomuchafua. Kwa maana ni ndani ya mutu, ni kusema ndani ya moyo wake, ndimo munamotoka mawazo mabaya yanayoleta: uzinzi, wizi, uuaji, uasherati, tamaa mbaya, matendo mabaya, ukorofi, maisha ya ovyo, wivu, matukano, majivuno na upumbafu. Maovu haya yote yanatoka ndani ya mutu, nayo yanamufanya kuwa muchafu.” Kisha Yesu akaondoka pale, na kwenda katika jimbo lililokuwa karibu na muji Tiro. Akaingia ndani ya nyumba, naye hakutaka mutu ajue kwamba yuko mule, lakini haikuwezekana kwake kujificha. Mwanamuke mumoja, binti yake aliyeshikwa na pepo, akasikia habari za Yesu. Mara moja akamufikia Yesu na kujitupa kwa miguu yake. Mwanamuke yule hakukuwa wa taifa la Wayuda. Alikuwa muzaliwa wa jimbo la Foinikia, katika inchi ya Suria. Yeye akamwomba Yesu afukuze yule pepo kutoka ndani ya binti yake. Lakini Yesu akamujibu: “Uwaache kwanza watoto wa nyumba washibe, kwa sababu si vizuri kukamata chakula cha watoto na kukitupia imbwa.” Mwanamuke yule akamujibu: “Bwana, unasema ukweli, lakini hata imbwa wanazoea kula makombo watoto wanayoyaangusha chini ya meza.” Basi Yesu akamwambia: “Kwa sababu ya jibu hili, unaweza kurudi kwako, yule pepo ametoka ndani ya binti yako.” Mwanamuke yule alipofika kwake, akamwona binti yake akilala katika kitanda; na yule pepo alikuwa amekwisha kutoka ndani yake. Kisha Yesu akaondoka kule katika jimbo lililokuwa karibu na Tiro, akapita Sidona na katikati ya inchi ya Miji Kumi, hata akafika kwenye ziwa la Galilaya. Wakamuletea mutu mumoja aliyekuwa kiziwi na mwenye kigugumizi vilevile. Wale waliomuleta wakamusihi Yesu amuponyeshe kwa kuweka mikono juu yake. Basi Yesu akamwondoa yule mutu kati ya kundi, akaenda naye mbali kidogo, akamutia vidole ndani ya masikio, akatema mate na kumugusa ulimi kwa mate yale. Kisha Yesu akaangalia juu mbinguni, akasisimua na kumwambia yule mutu: “Efata,” maana yake, “Funguka!” Mara moja masikio yake yakafunguka, nao ulimi wake ukafunguliwa, akaanza kusema vizuri. Yesu akawaagiza wasimwambie mutu habari ya tendo hili. Lakini kwa kadiri alivyowakataza, wao walizidi kutangaza habari. Nao watu wakashangaa sana na kusema: “Mambo anayofanya ni mazuri kweli. Anawawezesha hata viziwi wasikie, nao wabubu wapate kusema.” Katika siku zile kundi kubwa la watu walikusanyika tena. Nao walipokosa chakula, Yesu akawaita wanafunzi wake, na kuwaambia: “Ninawasikilia watu hawa huruma, kwa sababu wamekaa nami sasa muda wa siku tatu, nao hawana chakula tena. Kama nikiwaambia waende kwao pasipo kula wataregea katika njia, kwa maana wamoja kati yao wametoka mbali.” Wanafunzi wake wakamujibu: “Hapa katika pori mutu ataweza kupata wapi chakula cha kuwashibisha?” Yesu akawauliza: “Muko na mikate ngapi?” Nao wakamujibu: “Tuko na mikate saba.” Basi Yesu akawaamuru watu waikae chini. Kisha akakamata ile mikate saba, akamushukuru Mungu, akaimega na kuwapa wanafunzi wake waigawanye kwa watu; nao wanafunzi wakaigawanya. Walikuwa vilevile na samaki ndogo chache. Yesu akamushukuru Mungu na kuwaambia wanafunzi wazigawanye vilevile. Wote walikula na kushiba. Kisha wanafunzi wakaokota vipande vya mikate na vya samaki vilivyobaki, wakajaza vitunga saba. Watu waliokula walikuwa yapata elfu ine. Kisha kuagana nao, mara moja Yesu akaingia ndani ya chombo pamoja na wanafunzi wake, akaenda katika jimbo la Dalmanuta. Wafarisayo wakamufikia Yesu na kuanza kubishana naye. Wakamupima wakimwomba awaonyeshe kitambulisho kinachohakikisha kwamba uwezo wake umetoka kwa Mungu. Yesu akaugua sana kwa huzuni, na kusema: “Sababu gani ninyi watu wa kizazi hiki munataka kuona kitambulisho? Kweli ninawaambia, hamutaonyeshwa kitambulisho!” Kisha akawaacha, akaingia tena ndani ya chombo, akaanza kuvuka ziwa. Wanafunzi walikuwa wamesahau kupeleka mikate, isipokuwa walikuwa na mukate mumoja tu ndani ya chombo. Yesu akawaagiza: “Mujiangalie vizuri, mujiepushe na chachu ya Wafarisayo na ya Herode.” Wanafunzi wakaanza kusemezana: “Anasema hivi kwa sababu hatuna mikate.” Yesu akatambua maneno waliyosema, basi akawauliza: “Sababu gani munasemezana juu ya kukosa mikate? Hamujafahamu wala kuelewa? Mioyo yenu ingali migumu? Muko na macho, lakini hamwoni? Muko na masikio, lakini hamusikii? Hamukumbuki wakati nilipomega mikate mitano na kulisha watu elfu tano? Wakati ule mulijaza vitunga ngapi na vipande vya mikate?” Wakajibu: “Kumi na viwili.” Naye akawauliza tena: “Na wakati nilipomega mikate saba na kulisha watu elfu ine, mulijaza vitunga ngapi na vipande vya mikate?” Wakamujibu: “Saba.” Basi Yesu akawauliza: “Na hata sasa hamujaelewa kitu?” Yesu na wanafunzi wake wakafika Betesaida. Kule wakamuletea Yesu mutu mumoja kipofu na kumwomba amuguse kusudi apate kupona. Yesu akashika mukono wa yule kipofu na kumupeleka inje ya kijiji. Yesu alipokwisha kupakaa mate kwa macho ya mutu yule na kuweka mikono juu yake, akamwuliza: “Unaona kitu?” Kipofu akainua macho yake na kusema: “Ninaona watu wakitembea, lakini wanaonekana kama miti.” Yesu akagusa tena macho ya yule kipofu, naye akapata kuona vizuri. Macho yake yakapona, na kupata kuona vitu vyote waziwazi. Kisha Yesu akamwomba arudie kwake, akimwagiza asirudi katika kijiji. Yesu na wanafunzi wake wakaenda pande za vijiji vilivyokuwa karibu na muji Kaisaria Filipi. Walipokuwa katika njia yeye akawauliza: “Watu wanasema kwamba mimi ni nani?” Nao wakamujibu: “Wamoja wanasema kwamba wewe ni Yoane Mubatizaji; wengine wanasema kwamba wewe ni nabii Elia na wengine wanasema kwamba wewe ni mumoja wa manabii wengine.” Halafu Yesu akawauliza: “Na ninyi munasema kwamba mimi ni nani?” Petro akamujibu: “Wewe ni Kristo.” Basi Yesu akawaagiza wasimwambie mutu neno lile. Kisha Yesu akaanza kuwafundisha wanafunzi wake, akisema: “Sherti Mwana wa Mutu ateswe na kukataliwa na wasimamizi wa watu, wakubwa wa makuhani pamoja na walimu wa Sheria. Atauawa na kwa siku ya tatu kisha kufa kwake atafufuka.” Yeye aliwaambia maneno hayo waziwazi. Basi Petro akamwita Yesu pembeni na kuanza kumukaripia. Lakini Yesu akawageukia wanafunzi wake na kumukaripia Petro akisema: “Ondoka hapa karibu nami wewe Shetani, kwa maana mawazo yako si ya Mungu lakini ni ya kimutu.” Kisha Yesu akaita kundi la watu pamoja na wanafunzi wake, na kuwaambia: “Kama mutu akitaka kunifuata, asijishugulikie mwenyewe, lakini ajitolee kwa kubeba musalaba wake na kunifuata. Kwa maana mutu anayetaka kulinda uzima wake, ataupoteza; lakini yule atakayetoa uzima wake kwa ajili yangu na kwa ajili ya Habari Njema, ataulinda. Ni faida gani kwa mutu kupata utajiri wote wa dunia, lakini anapoteza uzima wake? Hakuna kitu chochote mutu anachoweza kutoa kwa kukomboa uzima wake. Kwa hiyo mutu yeyote anayesikia haya juu yangu na juu ya mafundisho yangu kati ya watu wa kizazi hiki kisichokuwa na uaminifu mbele ya Mungu na chenye zambi, Mwana wa Mutu atasikia haya juu yake vilevile. Itakuwa vile, atakapokuja pamoja na wamalaika watakatifu, akitukuzwa na Baba yake.” Na Yesu akaongeza kusema: “Kweli ninawaambia: wamoja kati ya watu wanaokuwa hapa hawatakufa mbele hawajaona Ufalme wa Mungu ukikuja kwa uwezo.” Nyuma ya siku sita, Yesu aliwatwaa Petro, Yakobo na Yoane, na kuwapeleka kwenye mulima murefu pekee yao. Na kule sura ya Yesu ikageuka mbele yao. Nguo zake zikageuka nyeupe sana na kumetameta, wala katika dunia hakuna fundi wa kufua anayeweza kuziangarisha kama vile. Halafu wale wanafunzi watatu wakawaona Elia na Musa wakisemezana na Yesu. Basi Petro akamwambia Yesu: “Mwalimu, ni vizuri kuona kwamba sisi tuko hapa. Tujenge vibanda vitatu, kimoja chako, kimoja cha Musa na kingine cha Elia.” Petro hakujua la kusema kwa maana yeye na wenzake waliogopa. Halafu wingu likatokea na kuwafunika, na sauti ikasikilika toka katikati ya lile wingu ikisema: “Huyu ni Mwana wangu mupendwa. Mumusikilize!” Mara moja wanafunzi waliangalia pande zao zote, hawakumwona mutu mwingine pamoja nao, isipokuwa Yesu peke yake. Walipokuwa wakishuka toka kwa mulima, Yesu akawaamuru: “Musimwelezee mutu mambo muliyoona mpaka Mwana wa Mutu atakapofufuka.” Wao walitii agizo hilo, lakini wakaanza kuulizana: “Maana ya kufufuka huku ni gani?” Kisha wakamwuliza Yesu: “Kwa nini walimu wa Sheria wanasema kama sherti Elia arudi kwanza?” Yesu akawajibu: “Hakika Elia anapaswa kurudi kwanza kutengeneza mambo yote. Lakini sababu gani Maandiko Matakatifu yanasema vilevile kwamba Mwana wa Mutu atateswa sana na kuzarauliwa? Lakini ninawaambia kama Elia amekwisha kurudi, na watu walimutendea yote waliyotaka, kama Maandiko yanavyosema juu yake.” Waliporudi kwenye wanafunzi wengine, wakaona kundi la watu wengi wakiwazunguka na walimu wa Sheria wakibishana nao. Mara moja, watu walipomwona Yesu, wakashangaa sana, wakakimbia kwenda kumusalimia. Yesu akawauliza wanafunzi wake: “Munabishana nao juu ya nini?” Na mutu mumoja kati ya kundi akamujibu: “Mwalimu, nimemuleta mwana wangu kwako, kwa maana yuko na pepo wa bubu. Kila wakati yule pepo anapomukamata, anamwangusha chini, na mutoto anatoka pofu na kusaga meno, nao mwili wake unakauka. Niliomba wanafunzi wako wamufukuze yule pepo, lakini hawakuweza.” Yesu akawaambia wanafunzi wake: “Ee ninyi watu wa kizazi kisichoamini Mungu! Nitakaa pamoja nanyi tena mpaka wakati gani? Nitawavumilia tena mpaka wakati gani? Muniletee mutoto hapa.” Halafu wakamuleta mutoto kwake. Na mara moja yule pepo alipomwona Yesu, akamutikisatikisa yule mutoto kwa nguvu hata akaanguka chini, akagaagaa chini na kutoka pofu. Yesu akamwuliza baba ya mutoto: “Amekuwa na hali hii tangu wakati gani?” Baba yake akamujibu: “Ni tangu utoto wake. Na mara nyingi huyu pepo anamutupa katika moto na ndani ya maji, kusudi amwue. Lakini kama unaweza kufanya kitu, utuhurumie na kutusaidia.” Yesu akamwambia: “Kwa sababu gani unasema: ‘Kama unaweza?’ Yote yanawezekana kwa yule anayeamini.” Mara moja baba ya mutoto akasema kwa nguvu: “Ninaamini! Lakini unisaidie kwa ajili ya kukosa kuamini!” Wakati Yesu alipoona watu wengi wanazidi kukusanyika mbiombio, akamukaripia yule pepo na kumwambia: “Wewe pepo wa bubu na wa kiziwi, ninakuamuru utoke ndani ya mutu huyu wala usimurudilie tena!” Yule pepo akalalamika, akamutikisatikisa mutoto kwa nguvu na kutoka ndani yake. Mutoto akaonekana sawa amekufa, hata watu wengi wakaanza kusema kwamba amekufa. Lakini Yesu akamushika mukono, akamwinua, naye akasimama. Yesu alipokwisha kuingia ndani ya nyumba, wanafunzi wake wakamwuliza hivi wakiwa peke yao: “Sababu gani sisi hatukuweza kumufukuza yule pepo?” Yesu akawajibu: “Pepo wa namna hii wanaweza kufukuzwa tu kwa njia ya maombi.” Yesu na wanafunzi wake wakatoka kule na kupitia jimbo la Galilaya. Yesu hakutaka mutu ajue pahali walipokuwa, kwa sababu alikuwa akiwafundisha wanafunzi wake, akiwaambia: “Mwana wa Mutu atatolewa katika mikono ya watu, nao watamwua, na kwa siku ya tatu kisha kufa kwake, atafufuka.” Lakini wanafunzi hawakufahamu maana ya mafundisho hayo. Wakaogopa kumwuliza neno. Walipofika Kapernaumu na kuingia ndani ya nyumba, Yesu akawauliza wanafunzi wake: “Mulibishana juu ya nini katika njia?” Lakini wakanyamaza, kwa sababu walikuwa wakibishana katika njia kwamba nani anayekuwa mukubwa kati yao. Basi Yesu akaikaa, akawaita wanafunzi wake kumi na wawili na kuwaambia: “Mutu anayetaka kuwa wa kwanza anapaswa kujiweka wa mwisho kuliko wote na kuwa mutumishi wa wote.” Kisha akatwaa mutoto mudogo, akamuweka mbele yao na kumukumbatia. Naye akawaambia: “Anayemupokea mutoto mudogo kama huyu kwa ajili yangu, ananipokea mimi. Na anayenipokea, hanipokei mimi tu, lakini anamupokea vilevile yule aliyenituma.” Yoane akamwambia Yesu: “Mwalimu, tulimwona mutu mumoja akifukuza pepo kwa jina lako, nasi tulimukataza kwa sababu yeye si wa kikundi chetu.” Lakini Yesu akajibu: “Musimukataze, kwa maana hakuna mutu anayefanya miujiza kwa jina langu, ambaye anaweza nyuma kidogo kusema vibaya juu yangu. Ni vile kwa maana asiyekuwa adui yetu, ni wa upande wetu. Na yeyote atakayewapa kikombe cha maji kwa ajili yangu, kwa sababu ninyi ni watu wa Kristo, kweli ninawaambia, mutu yule hatakosa kupewa zawadi yake.” “Yeyote atakayeangusha mumoja wa hawa wadogo wanaoniamini, ingelikuwa heri afungiwe jiwe kubwa la kusagia katika shingo na kutupwa ndani ya bahari. Kama mukono wako ukikukosesha, uukate! Ni heri kwako kuingia kwenye uzima wa kweli ukiwa na mukono mumoja, kuliko kuwa na mikono miwili na kwenda katika jehenamu ndani ya moto usiozimika. [ Mule muna vidudu visivyokufa, na moto usiozimika.] Kama muguu wako ukikukosesha, uukate. Ni heri kwako kuingia kwenye uzima wa kweli ukiwa na muguu mumoja, kuliko kuwa na miguu miwili na kutupwa katika moto wa jehenamu. [ Mule muna vidudu visivyokufa, na moto usiozimika.] Kama jicho lako likikukosesha, uliongoe. Ni heri kwako kuingia katika Ufalme wa Mungu ukiwa na jicho moja, kuliko kuwa na macho mawili na kutupwa katika jehenamu. Mule muna vidudu visivyokufa, na moto usiozimika. “Kwa maana kila mutu atatiwa chumvi kwa moto. “Chumvi ni kitu kizuri. Lakini chumvi ikipoteza onjo lake, itatiwa nini kusudi ipate tena kukolea? “Muwe na chumvi ndani yenu na muishi pamoja kwa amani.” Yesu akaondoka kule, akaenda katika jimbo la Yudea na kuvuka ngambo ingine ya Yordani. Na makundi mengi ya watu wakakusanyika tena mbele yake, naye akaanza kuwafundisha, kama vile alivyozoea kufanya. Wafarisayo wamoja wakamufikia kwa kumupima, wakamwuliza: “Sheria yetu inamuruhusu mutu kufukuza muke wake?” Yesu akajibu: “Musa aliwaamuru nini?” Nao wakamujibu: “Musa alitoa ruhusa kwa mutu kuandika barua ya kuachana na muke wake na kisha amufukuze.” Yesu akawaambia: “Musa aliwaandikia amri ile kwa sababu ya ugumu wa mioyo yenu. Lakini wakati Mungu alipowaumba watu wa kwanza, aliwaumba mwanaume na mwanamuke. Kwa sababu hii, mutu atawaacha baba yake na mama yake na kuungana na muke wake, nao wawili watakuwa mwili mumoja. Hivi wao si wawili tena, lakini wanakuwa mumoja. Basi mutu asitenganishe kile Mungu alichokiunganisha.” Walipokuwa ndani ya nyumba, wanafunzi wakamwuliza Yesu tena juu ya neno lile. Yesu akawaambia: “Kila mutu anayemufukuza muke wake na kuoa mwingine, anazini na kumukosea yule muke wa kwanza. Vile vile, kila muke anayemwacha mume wake na kuolewa na mwingine, anazini.” Watu wamoja wakamuletea Yesu watoto kusudi awawekee mikono, lakini wanafunzi wake wakawakaripia watu wale. Yesu alipoona vile, akakasirika na kuwaambia wanafunzi wake: “Muwaache watoto wadogo wakuje kwangu wala musiwakataze, kwa maana Ufalme wa Mungu ni wa watu wanaokuwa sawasawa na wao. Kweli ninawaambia ninyi: mutu yeyote asiyepokea Ufalme wa Mungu kama mutoto mudogo, hawezi kuingia ndani yake hata kidogo.” Kisha akawakumbatia watoto wale, akaweka mikono juu yao na kuwabariki. Yesu alipoondoka kwa kuendelea na safari yake, mutu mumoja akamufikia mbio akapiga magoti mbele yake na kumwuliza: “Mwalimu mwema, nifanye nini kusudi nipate kurizi uzima wa milele?” Yesu akamwuliza: “Sababu gani unaniita mwema? Hakuna mutu anayekuwa mwema, isipokuwa Mungu peke yake. Unajua jinsi amri zinavyosema kwamba: ‘Usiue, usizini, usiibe, usishuhudie uongo, usidanganye, uwaheshimu baba yako na mama yako.’ ” Yule mutu akamujibu: “Mwalimu, nimetii amri zile zote tangu ujana wangu.” Yesu akamwangalia kwa upendo, akamwambia: “Unakosewa na kitu kimoja tu: kwenda uuzishe vitu vyote unavyokuwa navyo, na uwape wamasikini mali zile, nawe utakuwa na akiba mbinguni. Kisha urudi, unifuate!” Lakini kijana yule aliposikia maneno yale, alikunja uso, na kujiendea katika huzuni, kwa sababu alikuwa tajiri sana. Yesu akaangalia pande zake zote na kuwaambia wanafunzi wake: “Kweli ni vigumu sana kwa watajiri kuingia katika Ufalme wa Mungu!” Wanafunzi wakashangaa sana kusikia maneno hayo. Lakini Yesu akawaambia tena: “Watoto wangu, ni vigumu kabisa kuingia katika Ufalme wa Mungu! Ni kwepesi zaidi kwa ngamia kupita katika tundu la sindano kuliko tajiri kuingia katika Ufalme wa Mungu.” Wanafunzi waliposikia maneno hayo wakazidi kushangaa hata wakaulizana wao kwa wao: “Ni nani basi anayeweza kuokolewa?” Yesu akawaangalia na kuwaambia: “Kwa mwanadamu haiwezekani, lakini kwa Mungu si vile, kwa maana mambo yote yanawezekana kwa Mungu.” Petro akamwambia: “Angalia sisi tumeacha vyote na kukufuata wewe!” Yesu akajibu: “Kweli ninawaambia: kama mutu akiacha nyumba yake, ndugu, dada, mama, baba, watoto wake au mashamba yake kwa ajili yangu na kwa ajili ya Habari Njema, atapokea mara mia zaidi katika wakati wa sasa. Atapokea nyumba, ndugu, dada, mama, watoto na mashamba pamoja na mateso. Na katika wakati utakaokuja atapokea uzima wa milele. Lakini wengi wanaokuwa wa kwanza watakuwa wa mwisho, na wengi wanaokuwa wa mwisho watakuwa wa kwanza.” Yesu na wanafunzi wake walipokuwa katika njia, wakipanda kwenda Yerusalema, yeye akatangulia mbele yao. Wanafunzi walishikwa na hofu, nao watu waliowafuata waliogopa. Yesu akawatwaa tena wanafunzi wake kumi na wawili, na kuanza kusemezana nao juu ya mambo yatakayomupata. Akawaambia: “Tunapanda kwenda Yerusalema na kule Mwana wa Mutu atatolewa kwa wakubwa wa makuhani na kwa walimu wa Sheria. Nao watamuhukumu auawe na kumutoa katika mikono ya watu wa mataifa mengine. Nao watamuchekelea, watamutemea mate, watamupiga fimbo na kumwua. Lakini kwa siku ya tatu kisha kufa kwake, atafufuka.” Kisha wana wawili wa Zebedayo, Yakobo na Yoane, wakamufikia Yesu na kumwambia: “Mwalimu, tunataka utufanyie jambo tutakalokuomba.” Yesu akawauliza: “Munataka niwafanyie nini?” Nao wakamujibu: “Utakapokuwa katika utukufu wako, uturuhusu kuikaa pamoja nawe, mumoja kwa upande wako wa kuume na mwingine kwa upande wako wa kushoto.” Lakini Yesu akawaambia: “Hamujui kitu munachoomba. Munaweza kunywa kikombe cha mateso nitakachokunywa? Au munaweza kubatizwa kwa namna ya ubatizo nitakaoupata?” Nao wakamujibu: “Tunaweza.” Yesu akaongeza kuwaambia: “Hakika mutakunywa kikombe nitakachokunywa, na kubatizwa kama vile nitakavyobatizwa. Lakini kuikalisha mutu kwa upande wangu wa kuume au wa kushoto si kazi yangu. Ni Mungu peke yake atakayeweka watu aliowatayarisha kwenye nafasi zile.” Wanafunzi wengine kumi waliposikia maneno yale, wakachukizwa na Yakobo na Yoane. Yesu akawaita wote na kuwaambia: “Munajua kwamba wale wanaohesabiwa kuwa watawala wa mataifa wanayatawala kwa kinguvu, na wakubwa yao wanayagandamiza. Lakini isikuwe hivi katikati yenu. Anayetaka kuwa mukubwa kati yenu, sherti akuwe mutumishi wenu. Naye anayetaka kuwa wa kwanza, sherti akuwe mutumwa wa wote. Kwa maana hata Mwana wa Mutu hakuja kutumikiwa, lakini kutumika na kutoa maisha yake kusudi awakomboe watu wengi.” Wakafika Yeriko. Na wakati Yesu alipokuwa akitoka kule pamoja na wanafunzi wake na kundi kubwa la watu, mutu mumoja kipofu aliyeitwa Bartimayo mwana wa Timayo, alikuwa akiikaa pembeni ya njia akiombaomba. Naye aliposikia kwamba Yesu wa Nazareti anapita katika njia ile, akalalamika, akisema: “Yesu Mwana wa Daudi, unisikilie huruma!” Watu wengi walimukaripia na kumwambia anyamaze, lakini alizidi kulalamika akisema: “Yesu Mwana wa Daudi, unisikilie huruma!” Yesu akasimama na kusema: “Mumwite.” Basi wakamwita yule kipofu na kumwambia: “Ujipe moyo! Simama, anakuita.” Bartimayo akatupa koti yake, akaruka upesi na kumwendea Yesu. Yesu akamwuliza: “Unataka nikufanyie nini?” Yule kipofu akamujibu: “Mwalimu, ninataka nipate kuona.” Yesu akamwambia: “Ujiendee, imani yako imekuponyesha.” Na pale pale akapata kuona, na kumufuata Yesu katika njia. Yesu na wanafunzi wake wakakaribia kufika Yerusalema, upande wa kijiji cha Betefage na cha Betania, karibu na mulima wa Mizeituni. Yesu akawatuma wawili katika wanafunzi wake, akiwaambia: “Mwende katika kijiji kinachokuwa mbele yenu. Wakati mutakapofika kule, mutaona mwana-punda amefungwa, na hakuna mutu aliyekwisha kupanda juu yake. Mumufungue na kumuleta hapa. Na kama mutu akiwauliza: ‘Kwa sababu gani munafanya hivi? Mumwambie kwamba Bwana yuko na lazima ya kumutumia, atamurudisha hapa nyuma kidogo.’ ” Basi wakaenda, wakaona mwana-punda amefungwa inje, karibu na mulango wa nyumba pembeni ya barabara. Walipokuwa wakimufungua, watu waliokuwa pale wakawauliza: “Munafanya nini? Kwa nini munamufungua mwana-punda huyu?” Wakawajibu sawa vile Yesu alivyowaambia, nao watu wale wakawaruhusu kwenda. Wakamuletea Yesu yule mwana-punda na kutandika nguo zao juu yake. Kisha Yesu akaikaa juu yake. Watu wengi wakatandika nguo zao katika njia na wengine wakatandika matawi waliyokata katika mashamba. Watu waliotangulia mbele ya Yesu na wale waliofuata nyuma yake wakaanza kulalamika kwa sauti kubwa, wakisema: “Mungu asifiwe! Abarikiwe huyu anayekuja kwa jina la Bwana! Ubarikiwe ufalme unaokuja, ndio ufalme wa babu yetu Daudi! Mungu asifiwe juu mbinguni!” Yesu akafika Yerusalema na kuingia ndani ya hekalu. Alipokwisha kuangalia vitu vyote pande zote, akaondoka na kwenda Betania pamoja na wanafunzi wake kumi na wawili, kwa sababu ilikuwa imekwisha kuwa magaribi. Kesho yake, walipotoka Betania, Yesu akasikia njaa. Akaona kwa mbali muti wa tini wenye majani mengi. Basi akaenda kuangalia kama atapata matunda juu ya muti ule. Lakini alipofika karibu nao, hakuona kitu juu yake isipokuwa majani matupu, kwa sababu haikukuwa wakati wake wa kutoa matunda. Halafu Yesu akalaani muti ule, akisema: “Tangia sasa hata milele, mutu asipate tena tunda tokea juu yako.” Nao wanafunzi wake wakasikia maneno hayo aliyosema. Kisha wakafika Yerusalema. Yesu alipoingia ndani ya hekalu, akaanza kufukuza watu waliokuwa wakiuzishia na kununulia vitu vyao ndani ya hekalu. Akapindua meza za wale waliobadilisha feza na viti vya wachuuzi wa njiwa. Vilevile akawakataza watu kukatiliza na mizigo yao katika kiwanja cha hekalu. Kisha akawafundisha maneno haya: “Imeandikwa katika Maandiko Matakatifu: ‘Nyumba yangu itaitwa nyumba ya maombi kwa mataifa yote.’ Lakini ninyi mumeigeuza kuwa nafasi ya kukutania ya wanyanganyi!” Wakubwa wa makuhani na walimu wa Sheria walipopata habari hii, wakatafuta njia ya kumwua Yesu. Lakini walimwogopa, kwa sababu kundi lote la watu walishangaa na mafundisho yake. Ilipokuwa magaribi, Yesu na wanafunzi wake wakatoka katika muji ule. Kesho yake asubui, walipokuwa wakipita, wakaona ule muti wa tini, nao ulikuwa umekauka wote, hata mizizi yake. Petro akakumbuka mambo yaliyotokea mbele, akamwambia Yesu: “Mwalimu, angalia, ule muti wa tini ulioulaani umekauka.” Yesu akawaambia wanafunzi wake: “Mumwamini Mungu. Kweli ninawaambia: ‘Mutu anaweza kuuambia mulima huu kwamba uondoke hapa na kujitupa katika bahari.’ Na ikiwa anasema maneno yale bila shaka katika moyo wake, lakini akiamini kama jambo lile litafanyika, hakika litafanyika kwake. Ni kwa hiyo ninawaambia kwamba munapoomba kwa ajili ya hitaji la kitu fulani, mwamini kama mumekwisha kukipokea, na kwa njia hiyo mutakipewa. Na munaposimama kwa kuomba, mukiwa na neno na mutu mwingine, mumusamehe, kusudi Baba yenu anayekuwa mbinguni, awasamehe vilevile makosa yenu. [ Lakini musipowasamehe wengine, Baba yenu anayekuwa mbinguni hatawasamehe ninyi makosa yenu vilevile.]” Yesu na wanafunzi wake wakafika tena Yerusalema. Yesu alipokuwa akitembea katika hekalu, wakubwa wa makuhani, walimu wa Sheria pamoja na wasimamizi wa watu, wakamufikia. Wakamwuliza: “Unafanya mambo haya kwa mamlaka gani? Na ni nani aliyekupa mamlaka haya?” Yesu akawajibu: “Nitawauliza ulizo moja tu. Kama mukinijibu, mimi vilevile nitawaambia ni kwa mamlaka gani ninafanya mambo haya. Yoane alipata mamlaka ya kubatiza kutoka kwa nani? Kwa Mungu au kwa watu? Munijibu.” Nao wakaanza kupiga mafikiri pamoja na kusema: “Kama tukijibu kwamba mamlaka yake yalitoka kwa Mungu, atatuuliza: ‘Kwa sababu gani hamukumwamini?’ Vilevile hatuwezi kusema kama yalitoka kwa watu…” (Waliogopa kundi la watu kwa maana wote walisadiki kama Yoane alikuwa nabii wa kweli). Basi wakamujibu Yesu: “Hatujui.” Naye akawaambia: “Nami vilevile sitawaambia ninyi ni kwa mamlaka gani ninafanya mambo haya.” Kisha Yesu akaanza kusema maneno haya kwa wale wakubwa kwa njia ya mifano: “Mutu mumoja alipanda shamba la mizabibu, akalizungusha na upango, akatengeneza nafasi ya kukamulia matunda ya mizabibu na kujenga munara kwa ajili ya walinzi wa shamba. Kisha akalipangisha kwa walimaji, akaenda safari katika inchi ingine. Siku za mavuno zilipotimia, akamutuma mutumishi wake mumoja kwa wale walimaji kusudi wamupatie sehemu yake ya mavuno. Lakini wale walimaji wakamukamata yule mutumishi, wakamupiga na kumurudisha mikono mitupu. Mwenye shamba akatuma tena kwao mutumishi mwingine. Yule naye, wakamwumiza kwenye kichwa na kumutukana. Mwenye shamba akatuma tena kwao mutumishi mwingine, nao wakamwua. Na kisha akatuma wengine wengi, nao wale walimaji wakawapiga wamoja na kuwaua wengine. Mwenye shamba alibaki tu na mutu mumoja, naye alikuwa mwana wake mupendwa. Mwisho akamutuma kwao, akisema: ‘Ninajua kwamba watamuheshimu mwana wangu.’ Lakini wale walimaji walipomwona akikuja, wakasemezana: ‘Musimame! Huyu ndiye atakayerizi shamba hili. Basi tumwue, na shamba hili litakuwa urizi wetu!’ Basi wakamukamata yule mwana, wakamwua na kutupa maiti yake inje ya shamba.” Kisha Yesu akauliza: “Basi yule mwenye shamba la mizabibu atafanya nini? Yeye atakuja na kuwaua wale walimaji. Na kisha atawapatia walimaji wengine shamba lile. Hamujasoma bado Maandiko Matakatifu yanayosema: ‘Jiwe lililokataliwa na wajengaji limekuwa sasa jiwe kubwa la musingi. Ni Bwana aliyefanya jambo hili, nalo ni ajabu sana kwetu.’ ” Basi hao wakubwa wakatafuta kumukamata Yesu, kwa sababu walitambua kwamba alisema mufano huo juu yao. Lakini kwa sababu waliogopa kundi la watu, wakamwacha ajiendee. Wafarisayo wamoja na watu wamoja waliojiunga na Herode walitumwa kwa Yesu kusudi wamunase katika masemi. Walipomufikia, wakamwuliza: “Mwalimu, tunajua kwamba wewe ni mutu wa kweli. Vilevile haushuguliki na mafikiri ya mutu lakini unafundisha kwa ukweli njia Mungu anayoamuru kufuata. Utuambie basi, Sheria inaturuhusu kulipa kodi kwa Mufalme wa Roma au hapana? Ni sherti tulipe au hapana?” Lakini kwa kuwa Yesu alitambua kwamba wao ni wanafiki, akawaambia: “Sababu gani munanipima? Muniletee kikoroti kimoja cha feza hapa kusudi nikione.” Wakakileta kwake. Yesu akawauliza: “Sura hii na jina hili linaloandikwa hapa ni vya nani?” Wakamujibu: “Ni vya Mufalme wa Roma.” Halafu Yesu akawaambia: “Mumupe Mufalme wa Roma vinavyokuwa vyake, na Mungu vinavyokuwa vyake.” Nao wakashangaa sana juu ya jibu lake. Wasadukayo wamoja, ndio wale watu wanaosema kwamba wafu hawatafufuka, wakamufikia Yesu na kumwuliza: “Mwalimu, Musa alituamuru: ‘Mutu akiwa na ndugu yake, naye akikufa na kuacha muke wake bila mutoto, yule ndugu yake anapaswa kumwoa yule mujane na kumuzalia ndugu yake marehemu watoto.’ Basi kulikuwa wandugu saba. Wa kwanza alioa mwanamuke, lakini mutu yule akakufa bila kuacha mutoto. Ndugu wa pili akamwoa yule mwanamuke, naye akakufa vilevile bila kuacha mutoto. Na ikakuwa vile kwa ndugu wa tatu na hata kwa wote saba. Wote walimwoa yule mwanamuke, kila mumoja kisha kufa kwa mwenzake, lakini wakakufa bila kuacha watoto. Na kwa mwisho yule mwanamuke akakufa vilevile. Sasa, siku wafu watakapofufuka, muke yule atakuwa wa nani; kwa maana wote saba walikuwa wamemwoa?” Yesu akawajibu: “Mumedanganyika kwa sababu ya kutojua Maandiko Matakatifu wala uwezo wa Mungu. Kwa maana wafu watakapofufuka, wataishi kama vile wamalaika wanavyoishi katika mbingu; hawataoa wala kuolewa. Na juu ya kufufuka kwa wafu, hamujasoma katika kitabu cha Sheria ya Musa, yale maandiko yanayosema juu ya kichaka kilichowaka moto? Mungu alimwambia Musa: ‘Mimi ni Mungu wa Abrahamu, Mungu wa Isaka na Mungu wa Yakobo.’ ” Na Yesu akaendelea kuwaambia: “Mungu si Mungu wa waliokufa, lakini ni Mungu wa wanaokuwa wazima. Hivi ninyi munadanganyika kabisa.” Mwalimu mumoja wa Sheria alikuwa pale Yesu alipobishana na Wasadukayo. Yeye alitambua kwamba Yesu aliwajibu vizuri. Basi akamujongelea na kumwuliza: “Ni amri gani inayokuwa ya kwanza katikati ya amri zote?” Yesu akamujibu: “Amri ya kwanza katikati ya zote ni hii: ‘Sikia, wewe taifa la Waisraeli! Bwana Mungu wetu ndiye Bwana peke yake. Umupende Bwana Mungu wako kwa moyo wako wote, kwa roho yako yote, kwa akili yako yote na kwa nguvu yako yote.’ Na amri ya pili ni hii: ‘Umupende mwenzako kama vile unavyojipenda mwenyewe.’ Hakuna amri zingine kubwa kupita hizi.” Yule mwalimu wa Sheria akamwambia Yesu: “Ni vizuri, Ee Mwalimu! Umesema kweli kwamba Mungu ni mumoja peke yake wala hakuna mungu mwingine isipokuwa yeye. Na mutu anapaswa kumupenda Mungu kwa moyo wake wote, kwa akili yake yote na kwa nguvu yake yote, naye anapaswa kumupenda mwenzake kama vile anavyojipenda mwenyewe. Mambo hayo ni bora zaidi kuliko kumutolea Mungu nyama za kuteketezwa kwa moto na sadaka zingine zote.” Yesu alipoona kwamba amejibu kwa akili, akamwambia: “Si mbali kwako kuingia katika Ufalme wa Mungu.” Kisha maneno hayo hakuna mutu aliyesubutu tena kumwuliza Yesu neno. Yesu alipokuwa akifundisha katika hekalu akauliza: “Namna gani walimu wa Sheria wanaweza kusema kwamba Kristo ni Mwana wa Daudi? Daudi yeye mwenyewe, akiongozwa na Roho Mutakatifu, alisema: ‘Bwana wetu Mungu alimwambia Bwana wangu: Ikaa na mamlaka kwa kuume kwangu, mpaka nitakapoweka waadui zako chini ya miguu yako.’ Daudi mwenyewe anamwita Kristo ‘Bwana’; namna gani basi Kristo anaweza kuwa Mwana wake?” Kundi kubwa la watu walimusikiliza Yesu kwa furaha. Katika mafundisho yake aliwaambia: “Mujiepushe na walimu wa Sheria, wanaopenda kujitembeza wakivaa kanzu ndefu, na kusalimiwa kwa heshima kwenye nafasi ya makutano. Wanapenda vilevile kuikaa katika viti vya mbele ndani ya nyumba za kuabudia na kwenye nafasi za heshima katika karamu. Wananyanganya mali ya wajane na kuomba maombi marefu kusudi waonekane mbele ya watu. Kwa sababu hii watahukumiwa vikali sana!” Yesu akaikaa akielekea kwenye sanduku ya kutilia sadaka za hekalu. Akaangalia jinsi watu walivyotia feza ndani ya sanduku ile. Watajiri wengi walitia feza nyingi ndani yake. Na kukakuja mujane mumoja masikini, akatoa vikoroti viwili vidogo sana vinavyolingana na sengi mbili. Basi Yesu akawaita wanafunzi wake na kuwaambia: “Kweli ninawaambia kwamba mujane huyu masikini ametoa mingi zaidi kuliko wote wanaotia feza ndani ya sanduku ya sadaka. Kwa maana wengine wote walitoa sehemu ya mali wasiyokuwa nayo lazima. Lakini yeye ametoa kwa umasikini wake, mali yote aliyokuwa nayo kwa kuishi.” Yesu alipokuwa akitoka katika hekalu, mumoja kati ya wanafunzi wake akamwambia: “Mwalimu, angalia mawe haya mazuri na majengo haya makubwa!” Yesu akamujibu: “Unaona majengo haya makubwa? Hakutabaki hata jiwe moja juu ya lingine; yote yatabomolewa.” Yesu alipokuwa akiikaa kwa mulima wa Mizeituni kuelekea upande wa hekalu, Petro, Yakobo, Yoane na Andrea walipokuwa peke yao pamoja naye, wakamwuliza: “Utuambie, mambo hayo uliyotoka kusema yatakuwa wakati gani? Na ni kitambulisho gani kitakachoonyesha kwamba mambo hayo yote yanataka kutimia?” Basi Yesu akaanza kuwaambia: “Muangalie vizuri mutu asiwadanganye. Watu wengi watakuja wakijiita kwa jina langu, wakisema: ‘Mimi ni Kristo!’ Nao watawadanganya wengi. Mutakaposikia habari za matokeo au utetezi wa vita musiogope. Sherti mambo hayo yatukie, lakini hayaonyeshi kama mwisho umefika. Kwa maana taifa litapigana na taifa, na ufalme utapigana na ufalme. Kutakuwa tetemeko la inchi pahali mbalimbali. Vilevile kutakuwa njaa. Na haya yote ni kama mwanzo wa maumivu ya kuzaa tu. “Mujiangalie vizuri ninyi wenyewe, kwa maana watawapeleka mbele ya tribinali kwa kuwahukumu na kuwapiga fimbo katika nyumba za kuabudia. Vilevile mutapelekwa mbele ya wakubwa na wafalme kwa ajili yangu, kusudi mutoe ushuhuda wangu mbele yao. Ni lazima Habari Njema ihubiriwe kwanza kwa watu wa kila taifa. Na mutakapokamatwa na kupelekwa kwa kuhukumiwa, musijihangaishe mbele ya wakati juu ya maneno mutakayosema, lakini museme maneno mutakayopewa saa ile ile. Kwa sababu hayatatoka kwenu wenyewe, lakini yatatoka kwa Roho Mutakatifu. Ndugu atamutoa ndugu, kusudi auawe, na baba atatoa mutoto wake, nao watoto watawageukia wazazi wao na kuwaua. Na watu wote watawachukia kwa ajili yangu. Lakini atakayevumilia mpaka mwisho, ataokolewa. “Lakini mutamwona yule anayeitwa ‘Chukizo Linaloleta Uharibifu,’ akisimamishwa pahali asipopaswa kuwa. (Anayesoma maneno haya aelewe maana yake). Basi watakaokuwa Yudea, wakimbilie kwa milima. Atakayekutiwa juu ya paa la nyumba asishuke na kuingia ndani ya nyumba kutwaa kitu. Na mutu atakayekutiwa katika shamba, asirudi kwake kwa kutwaa nguo yake. Wanawake wenye mimba na wenye kunyonyesha watapata hasara katika siku zile. Mumwombe Mungu kusudi mambo hayo yasitokee katika wakati wa mvua. Kwa maana katika siku zile kutakuwa mateso makubwa yasiyoonekana hata kidogo tangu siku ile Mungu alipoumba ulimwengu mpaka sasa, wala hakutatokea tena mateso kama yale. Na kama Bwana asingepunguza siku zile za mateso, hakuna hata mutu mumoja ambaye angeponyoka kufa. Lakini kwa ajili ya wachaguliwa aliowachagua amezipunguza. “Kwa hiyo mutu akiwaambia: ‘Kristo yuko hapa!’ au ‘Yuko kule!’ musimusadiki. Kwa maana kutatokea watu wanaojiita kwa uongo ‘Kristo’ pamoja na manabii wa uongo, nao watafanya vitambulisho na maajabu, kusudi ikiwezekana wawadanganye wachaguliwa wa Mungu. Lakini ninyi mujiangalie vizuri, kwa maana nimewaambia hayo yote mbele. “Lakini katika siku zile kisha mateso yale, jua litatiwa giza, mwezi hautaangaza, nyota zitaanza kuanguka toka mbinguni na vyote vyenye nguvu vinavyokuwa katika mbingu vitatikiswa. Na halafu wakati ule Mwana wa Mutu ataonekana akikuja katikati ya mawingu kwa uwezo mwingi na kwa utukufu. Halafu atawatuma wamalaika wake katika pande ine za dunia, naye atakusanya watu wake aliowachagua kutoka katika dunia nzima. “Muangalilie mufano juu ya muti wa tini. Wakati matawi yake yanapochipuka, nayo majani yao yanapochipuka, ninyi munatambua kwamba wakati wa jua kali unakaribia. Vilevile, wakati mutakapoona mambo hayo niliyotoka kutaja yanatokea, mujue kwamba yeye yuko karibu, na amekuwa kwa mulango. Kweli ninawaambia: hiki kizazi chenu hakitapita mbele ya kutimia kwa mambo haya yote. Mbingu na dunia vitatoweka, lakini maneno yangu hayatabadilika hata kidogo. “Lakini hakuna mutu anayejua siku ile au saa, hata wamalaika wanaokuwa mbinguni, hata Mwana; isipokuwa Baba peke yake tu. Mujiangalie, mukeshe, kwa maana hamujui saa wakati ule utakapotimia. Itakuwa kama vile mutu anayefunga safari. Alipotoka kwake akawaachia watumishi madaraka yake, akimupa kila mutu kazi yake. Vilevile akamwagiza mulinzi wa mulango akeshe. Basi muangalie sababu hamujui wakati bwana wa nyumba atakaporudi: labda magaribi, au katikati ya usiku, au wakati jogoo anapowika, au asubui. Mujiangalie, asikuje kwa rafla na kuwakuta mumelala usingizi. Mambo ninayowaambia ninyi, ninayasema kwa wote: mukeshe.” Kulikuwa kumebaki siku mbili mbele ya kutimia kwa sikukuu ya Pasaka na ya Mukate Usiyotiwa Chachu. Wakubwa wa makuhani na walimu wa Sheria walitafuta njia ya kumukamata Yesu kwa werevu kusudi wamwue. Kwa maana walijisemesha: “Tusimukamate kwa wakati wa karamu, kusudi fujo isitokee kati ya watu.” Yesu alikuwa Betania katika nyumba ya mutu aliyeitwa Simoni Mukoma. Walipokuwa wakikula, mwanamuke mumoja akaingia ndani ya nyumba. Alikuwa na chupa la jiwe lenye marasi ya bei kali yaliyotengenezwa na maua ya nardo safi. Kisha akavunja mudomo wa lile chupa na kumimia marasi juu ya kichwa cha Yesu. Na wamoja kati ya watu waliokuwa pale wakachukizwa na kitendo kile na kusemezana: “Kwa nini kupoteza mali namna hii? Marasi hii ingeweza kuuzishwa kwa bei ya vikoroti mia tatu vya feza na kugawanyia wamasikini mali ile.” Na wakamukasirikia yule mwanamuke vikali. Lakini Yesu akasema: “Mumwache kimya! Sababu gani munamusumbua? Yeye amenitendea jambo zuri. Kwa maana mutakuwa na wamasikini pamoja nanyi siku zote, na munaweza kuwasaidia wakati wowote munapotaka, lakini mimi sitakuwa pamoja nanyi siku zote. Amefanya sawa alivyoweza. Ameupakaa mwili wangu marasi mbele ya wakati kwa kuutayarisha kwa ajili ya maziko. Kweli ninawaambia: kwa ajili ya kukumbuka mwanamuke huyu, tendo lile alilofanya litaelezwa popote Habari Njema itakapohubiriwa katika dunia nzima.” Yuda Iskariota, mumoja wa wanafunzi kumi na wawili, akaenda kwa wakubwa wa makuhani, kusudi amutoe Yesu kwao. Waliposikia habari ile wakafurahi sana, nao wakamwahidia kumupa feza. Basi Yuda akaanza kutafuta wakati muzuri kwa kumutoa. Siku ya kwanza ya karamu ya sikukuu ya Mukate Usiyotiwa Chachu, wakati ambapo walichinja kondoo wa Pasaka, wanafunzi wa Yesu wakamwuliza: “Unataka tuende wapi kukutayarishia karamu ya Pasaka?” Basi Yesu akawatuma wawili kati ya wanafunzi wake akiwaambia: “Mwende katika muji, na kule mutakutana mutu mumoja anayebeba mutungi wenye maji. Mumufuate mutu yule, na pahali atakapoingia, mumwambie mwenye nyumba: ‘Mwalimu anauliza kwamba ni wapi kunapokuwa chumba chake ambamo atakulia karamu ya Pasaka pamoja na wanafunzi wake.’ Naye atawaonyesha chumba kikubwa cha gorofi, kilichokwisha kupangwa vizuri na kuwa tayari. Ni mule mutakapotutayarishia karamu.” Halafu wanafunzi wakaondoka, wakaenda katika muji, wakakuta vitu vyote tayari sawa vile Yesu alivyowaambia. Nao wakatayarisha karamu ya Pasaka. Ilipokuwa magaribi, Yesu akafika pamoja na wanafunzi wake kumi na wawili. Walipokuwa wameikaa kula chakula, Yesu akasema: “Kweli ninawaambia: mumoja kati yenu anayekula pamoja nami atanitoa.” Wanafunzi wakaanza kuhuzunika na kumwuliza mumoja kwa mumoja: “Ni mimi?” Yesu akawajibu: “Ni mumoja kati yenu ninyi kumi na wawili, anayechovya mukate pamoja nami ndani ya sahani moja. Kwa maana Mwana wa Mutu atakufa sawa vile Maandiko Matakatifu yanavyosema juu yake, lakini ole kwa yule mutu atakayemutoa! Ingekuwa heri kwake kama asingezaliwa.” Walipokuwa wakikula, akatwaa mukate, akaubariki, kisha akaumega na kuwapa wanafunzi wake, akisema: “Mutwae, huu ni mwili wangu.” Kisha akatwaa kikombe, akakibariki na kuwapa, nao wote wakakikunywa. Na Yesu akawaambia: “Hii ni damu yangu; damu inayomwangika kwa ajili ya watu wengi kwa kuhakikisha agano la Mungu. Kweli ninawaambia: Tangia sasa sitakunywa tena divai mpaka siku ile nitakapoikunywa kwa upya katika Ufalme wa Mungu.” Na walipokwisha kuimba wimbo, wakaondoka kwenda kwa mulima wa Mizeituni. Yesu akawaambia wanafunzi wake: “Ninyi wote mutaanguka, kwa maana imeandikwa katika Maandiko Matakatifu: ‘Nitamwua muchungaji, na kondoo watasambazwa.’ Lakini nitakapokwisha kufufuka, nitawatangulia Galilaya.” Petro akamwambia: “Hata wote wengine wakianguka, mimi sitaanguka.” Yesu akamujibu: “Kweli ninakuambia kwamba usiku huu, mbele jogoo hajawika mara mbili, utakuwa umenikana mara tatu.” Lakini Petro akazidi kusema kwa nguvu: “Hata ikinipasa kufa pamoja nawe, sitakukana hata kidogo.” Na wote wengine wakasema sawasawa naye. Wakafika katika bustani inayoitwa Getesemane, na Yesu akawaambia wanafunzi wake: “Muikae hapa kwa wakati mimi nitakapokuwa nikiomba.” Kisha akatwaa Petro, Yakobo na Yoane na kwenda nao. Akaanza kuwa na hofu na mahangaiko. Akawaambia: “Ninahuzunika sana, karibu kufa! Mubakie hapa na mukeshe.” Kisha akajitenga mbali kidogo nao, akajitupa chini. Akaomba kwamba ikiwezekana, saa ile ya mateso imuondokee mbali. Akasema: “Ee baba! Yote yanawezekana kwako; ninakuomba uniondolee mbali hiki kikombe cha mateso. Lakini isikuwe kama vile mimi ninavyotaka, lakini kama vile wewe unavyotaka.” Aliporudi akawakuta wamelala usingizi. Akamwambia Petro: “Simoni, umelala? Haukuweza kukesha hata kwa saa moja tu? Mukeshe na kuomba, kusudi musianguke katika majaribu; kwa maana roho ni hodari, lakini mwili ni zaifu.” Mara tena akawaacha, akaomba akirudilia maneno yale yale. Aliporudi tena, akawakuta wanafunzi wale wamelala usingizi, kwa maana macho yao yalikuwa yamewezwa sana na usingizi. Nao hawakujua wamujibu nini. Aliporudi kwa mara ya tatu, akawaambia: “Mungali munalala na kupumzika? Inatosha! Saa imetimia. Sasa Mwana wa Mutu anatolewa katika mikono ya wenye zambi. Musimame, tuende! Yule anayenitoa, amefika karibu!” Yesu alipokuwa hajamaliza kusema, mara moja Yuda, mumoja wa wanafunzi kumi na wawili, akafika pamoja na kundi kubwa la watu wenye panga na magongo. Hawa wote walikuwa wametumwa na wakubwa wa makuhani, walimu wa Sheria, na wasimamizi wa watu. Yuda, yule aliyekuwa amemutoa, alikuwa amekwisha kuwapa kitambulisho hiki: “Yule nitakayemubusu, ndiye yeye. Mumukamate na mumupeleke, mukimulinda vizuri.” Yuda alipofika, mara moja akamujongelea Yesu na kumwambia: “Mwalimu!” Kisha akamubusu. Basi wale watu wakamukamata Yesu na kumufunga. Lakini mumoja kati ya wale waliokuwa pale, akachomoa upanga wake na kumukata mutumishi wa Kuhani Mukubwa sikio. Kisha Yesu akawaambia: “Mumekuja na panga na magongo kwa kunikamata kama watu wanavyokwenda kumukamata munyanganyi? Siku zote nilikuwa pamoja nanyi, nami nilifundisha ndani ya hekalu, nanyi hamukunikamata. Lakini mambo haya yamefanyika kusudi Maandiko Matakatifu yatimizwe.” Wanafunzi wake wote wakamwacha na kukimbia. Lakini kijana mumoja aliyevaa shuka akaendelea kumufuata Yesu. Walijaribu kumukamata, lakini akaachilia shuka ile na kukimbia uchi. Wakamupeleka Yesu mbele ya Kuhani Mukubwa, nao wakubwa wote wa makuhani, na wasimamizi wa watu pamoja na walimu wa Sheria wakakusanyika pale. Petro akamufuata Yesu kwa mbali, hata akaingia ndani ya upango wa nyumba ya Kuhani Mukubwa. Pale akaikaa pamoja na walinzi, akiota moto. Wakubwa wa makuhani na wakubwa wote wa Baraza Kubwa walitafuta mashitaki juu ya Yesu kusudi wapate kumwua, lakini hawakupata neno. Watu wengi walimushuhudia uongo, lakini ushuhuda wao haukupatana. Hata wengine wakasimama kwa kutoa ushuhuda huu wa uongo juu yake wakisema: “Sisi tulimusikia akisema: ‘Mimi nitabomoa hekalu hili lililojengwa na watu, na katika siku tatu nitajenga lingine lisilojengwa na watu.’ ” Lakini hata hivi ushuhuda wao haukupatana. Basi Kuhani Mukubwa akasimama katikati ya watu na kumwuliza Yesu: “Haujibu hata neno? Watu hawa wanakushitakia nini?” Lakini Yesu akanyamaza, wala hakujibu neno. Kuhani Mukubwa akamwuliza tena: “Wewe ndiwe Kristo, Mwana wa Mungu mwenye sifa?” Yesu akajibu: “Mimi Ndiye! Nanyi mutamwona Mwana wa Mutu akiikaa na mamlaka kwa kuume kwa Mungu Mwenye Uwezo. Mutamwona vilevile akikuja katika mbingu katikati ya mawingu!” Wakati Kuhani Mukubwa aliposikia maneno haya, akapasua nguo zake, na kusema: “Hatuhitaji tena ushuhuda wowote juu ya mutu huyu. Mumesikia wenyewe jinsi alivyomutukana Mungu. Munawaza nini?” Wote wakamuhukumu kwamba anastahili kufa. Wengine katikati yao wakaanza kumutemea Yesu mate, wakamufunika uso na kumupiga ngumi, wakimwambia: “Tambua sasa ni nani aliyekupiga!” Nao waaskari walinzi wakamukamata Yesu na kumupiga makofi. Petro alipokuwa angali chini ndani ya upango, mumoja wa watumishi wanawake wa Kuhani Mukubwa akafika pale. Alipomwona Petro akiota moto, akamwangalia, na kumwambia: “Wewe vilevile ulikuwa pamoja na Yesu wa Nazareti.” Lakini Petro akakana, akisema: “Sijui wala sifahamu maneno unayotaka kusema.” Kisha akatoka inje ya upango na kwenda kwenye kiingilio cha mulango. [Jogoo akawika.] Yule mutumishi mwanamuke akamwona pale, akaanza tena kuwaambia wale waliokuwa pale: “Huyu mutu ni mumoja wao!” Lakini Petro akakana tena. Nyuma kidogo, watu wale wakamwambia Petro tena: “Hakika wewe ni mumoja wao, kwa sababu wewe vilevile ni wa Galilaya.” Basi Petro akaanza kusema: “Nilaaniwe ikiwa ninasema uongo! Ninaapa kwamba simujui mutu huyu munayemutaja.” Mara moja jogoo akawika kwa mara ya pili, na Petro akakumbuka maneno yale Yesu aliyomwambia kwamba mbele jogoo hajawika mara mbili, atakuwa amemukana mara tatu. Basi akaanza kulia. Asubui mapema, mara moja wakubwa wa makuhani wakafanya shauri pamoja na wasimamizi wa watu, walimu wa Sheria na wakubwa wote wa baraza. Wakamufunga Yesu, wakamupeleka na kwenda kumutoa kwa Pilato. Pilato akamwuliza Yesu: “Wewe ni Mufalme wa Wayuda?” Yesu akamujibu: “Umesema.” Nao wakubwa wa makuhani wakamushitaki Yesu juu ya mambo mengi. Basi Pilato akamwuliza tena: “Wewe haujibu hata neno? Angalia mambo haya yote wanayokushitakia!” Lakini Yesu hakujibu neno lolote tena, hata Pilato akashangaa. Kila sikukuu ya Pasaka, Pilato alizoea kuwafungulia watu mufungwa mumoja, yule waliyemutaka. Kulikuwa mufungwa mumoja, jina lake Baraba, aliyefungwa pamoja na waasi wamoja kwa sababu ya uuaji na uasi walioufanya. Watu wakamwendea Pilato, wakaanza kumwomba awatendee kama ilivyokuwa desturi yake. Pilato akawajibu, akiwauliza: “Munataka niwafungulie ‘Mufalme wa Wayuda?’ ” Alisema vile kwa maana alitambua kwamba wakubwa wa makuhani wamemutoa Yesu kwa sababu walimwonea wivu tu. Lakini wakubwa wa makuhani wakawachochea watu wamwombe Pilato awafungulie Baraba. Pilato akawauliza watu tena: “Basi munataka nifanye nini na huyu munayemwita Mufalme wa Wayuda?” Wakapiga kelele tena wakisema: “Atundikwe juu ya musalaba!” Pilato akawauliza: “Alifanya ubaya gani?” Lakini wakazidi kupiga kelele wakisema: “Atundikwe juu ya musalaba!” Kwa kuwa Pilato alitaka kuwapendeza watu, basi akawafungulia Baraba. Na kisha kuamuru wamupige Yesu fimbo, akamutoa kusudi atundikwe juu ya musalaba. Waaskari wakamupeleka Yesu ndani ya upango wa nyumba ya liwali, nao wakaita kundi lao lote wakusanyike. Wakamuvalisha Yesu nguo nyekundu, na wakasokota taji na tawi lenye miiba na kumuvalisha nalo juu ya kichwa. Kisha wakaanza kumusalimia, wakisema: “Jambo, Mufalme wa Wayuda!” Wakamupigapiga tete juu ya kichwa, wakamutemea mate, wakapiga magoti na kuinama mbele yake. Walipokwisha kumuchekelea, wakamuvua ile nguo nyekundu na kumuvalisha nguo zake. Kisha wakaondoka naye inje kwa kwenda kumutundika juu ya musalaba. Mutu mumoja wa Kurene, aliyeitwa Simoni, baba ya Alesanduro na Rufu, alikuwa akipita katika njia, akitoka kwenye vijiji. Waaskari wakamushurutisha abebe musalaba wa Yesu. Wakamufikisha Yesu kwenye pahali palipoitwa Golgota, maana yake “Kilima cha Mufupa wa Kichwa.” Wakamupa divai iliyochanganywa na manemane, lakini akaikataa. Kisha wakamutundika juu ya musalaba, wakagawanyana nguo zake kwa kuzipigia kura, kusudi wajue nguo gani kila mumoja atakazopaswa kutwaa. Ilikuwa saa tatu ya asubui wakati walipomutundika juu ya musalaba. Na tangazo hili liliandikwa kwa kuonyesha sababu ya kuhukumiwa kwake. “Mufalme wa Wayuda.” Vilevile waliwatundika wanyanganyi wawili juu ya misalaba pamoja na Yesu, mumoja kwa upande wake wa kuume na mwingine kwa upande wa kushoto. [ Maandiko Matakatifu yanayosema hivi yakatimizwa: “Alihesabiwa pamoja na watenda mabaya.”] Watu waliokuwa wakipita pale walimutukana na kutikisatikisa vichwa vyao, wakisema: “Ewe! Wewe uliyetaka kubomoa hekalu na kujenga lingine katika siku tatu, ujiokoe sasa mwenyewe, ukijishusha juu ya musalaba!” Vilevile wakubwa wa makuhani na walimu wa Sheria kati yao walimusimanga Yesu, wakisemezana: “Aliokoa wengine, lakini sasa anashindwa kwa kujiokoa yeye mwenyewe! Kristo, Mufalme wa Waisraeli, ajishushe sasa juu ya musalaba, kusudi nasi tupate kuona na kumwamini.” Hata wale waliotundikwa pamoja naye walimutukana vilevile. Ilipokuwa saa sita ya muchana, giza likakuwa katika inchi yote mpaka saa tisa. Na saa tisa Yesu akalalamika: “Eloi, Eloi, lama sabaktani” maana yake “Mungu wangu, Mungu wangu, kwa nini umeniacha?” Na watu wamoja waliokuwa pale walipomusikia, wakasema: “Musikilize, anamwita Elia.” Na mumoja wao akaenda mbio, akachovya kikausho ndani ya divai yenye kuchacha na kukifungia juu ya tete. Kisha akakipandishia Yesu, kusudi apate kunywa, akisema: “Mwache tuone kama Elia atakuja kumushusha juu ya musalaba.” Lakini Yesu akalalamika kwa sauti kubwa, akakata roho. Basi pazia la hekalu likapasuka vipande viwili toka juu mpaka chini. Mukubwa wa waaskari aliyekuwa akisimama mbele ya Yesu, alipoona namna alivyokata roho, akasema: “Hakika mutu huyu alikuwa Mwana wa Mungu!” Kulikuwa wanawake wamoja walioangalia kwa mbali. Kati yao kulikuwa Maria wa Magdala, Maria mama ya kijana Yakobo na Yose na mwanamuke mwingine Salome. Wanawake hawa ni wale waliomufuata Yesu na kumushugulikia wakati alipokuwa Galilaya. Wanawake wengine wengi waliomufuata mpaka Yerusalema walikuwa pale vilevile. Pilato akashangaa sana kusikia kwamba Yesu amekwisha kufa. Basi akamwita yule mukubwa wa waaskari na kumwuliza kama kumepita muda murefu tangia Yesu alipokufa. Alipokwisha kuhakikishwa na yule mukubwa wa waaskari kwamba Yesu amekwisha kufa, akamuruhusu Yosefu atwae maiti yake. Yosefu akanunua vitambaa, akaondoa maiti ya Yesu juu ya musalaba, akaifungafunga na vile vitambaa na kuiweka ndani ya kaburi lililochimbwa ndani ya jiwe. Kisha wakasukumia jiwe kwenye kiingilio cha lile kaburi. Maria wa Magdala na Maria mama ya Yose walikuwa wakiangalia, pahali walipomuzika Yesu. Siku ya Sabato ilipokwisha kupita, Maria wa Magdala, na Maria mama ya Yakobo, na mwanamuke mwingine Salome, walinunua marasi kusudi waende kupakaa maiti ya Yesu. Siku ya kwanza ya juma, asubui mapema, wakati jua lilipoanza kutokea, wakaenda kwenye kaburi. Nao walienda wakiulizana: “Ni nani atakayetusukumia lile jiwe kutoka kwenye kiingilio cha kaburi?” Lakini walipoinua macho, wakaona kwamba lile jiwe lilikuwa limekwisha kusukumwa pembeni. (Jiwe lile lilikuwa kubwa sana.) Basi wakaingia ndani ya kaburi, na mule wakaona kijana mumoja akiikaa upande wa kuume, akivaa kanzu nyeupe. Nao wakashituka. Lakini kijana yule akawaambia: “Musishituke! Munamutafuta Yesu wa Nazareti aliyetundikwa juu ya musalaba. Yeye amefufuka, hayuko hapa. Muangalie, hapa ni pahali walipomuweka. Muende sasa kupasha habari kwa wanafunzi wake na kwa Petro, muwaambie kwamba anawatangulia Galilaya; nao watamwona kule sawa vile alivyowaambia.” Basi walitoka kwenye kaburi na kukimbia mbio. Walikuwa wakitetemeka na kushangaa sana. Nao hawakumwambia mutu yeyote, kwa sababu waliogopa. [ Yesu alipokwisha kufufuka asubui mapema, siku ya kwanza ya juma, alimutokea kwanza Maria wa Magdala, yule aliyefukuza pepo saba toka ndani yake. Huyu akaenda kupasha habari kwa wale waliokuwa wakikaa pamoja na Yesu. Walikuwa wakiomboleza na kulia. Na waliposikia jinsi Maria alivyowaambia kwamba Yesu ni muzima, na kwamba amemwona, hawakumusadikia. Kisha, Yesu akawatokea wanafunzi wawili, akiwa na sura ingine. Wanafunzi hao walikuwa wanakwenda kwenye vijiji. Nao wakarudi na kuwapasha wanafunzi wengine habari ile, lakini wao vilevile hawakusadikia. Kwa mwisho Yesu akawatokea wanafunzi kumi na mumoja walipokuwa wakikula. Naye akawakaripia kwa sababu ya kutokuamini kwao na kwa sababu ya ugumu wao. Kwa maana hawakusadikia wale waliomwona nyuma ya kufufuka kwake. Kisha akawaambia: “Mwende katika dunia yote na kuhubiri Habari Njema kwa kila mutu. Anayeamini na kubatizwa ataokolewa, lakini asiyeamini atahukumiwa. Nao wote watakaoniamini watafanya vitambulisho hivi: watafukuza pepo kwa jina langu; watasema kwa luga mupya; wakishika nyoka au kunywa sumu yoyote, hawatakufa. Wataweka mikono yao juu ya wagonjwa, nao watapona.” Bwana Yesu alipokwisha kusema nao maneno hayo, akanyanyuliwa juu kwenda mbinguni na kuikaa kwa upande wa kuume wa Mungu. Nao wanafunzi wakaenda kuhubiri fasi zote. Bwana akatumika pamoja nao na kuhakikisha ukweli wa mahubiri yao kwa njia ya vitambulisho walivyofanya.] kusudi upate kujua ukweli juu ya mambo uliyofundishwa. Katika siku Herode alipokuwa mufalme wa Yudea, kulikuwa kuhani mumoja, aliyeitwa Zakaria, wa kundi la makuhani wa ukoo wa Abiya. Muke wake Elizabeti alikuwa vilevile wa uzao wa Kuhani Mukubwa Haruni. Wote wawili walikuwa wenye haki mbele ya Mungu, walishika kwa ukamilifu amri na maagizo yote ya Bwana. Lakini hawakukuwa na mutoto, kwa maana Elizabeti alikuwa tasa, tena wote wawili walikuwa wazee sana. Siku moja, Zakaria alikuwa akimutumikia Mungu, akifanya kazi yake ya ukuhani kwa maana ilikuwa zamu ya kundi lake. Na kama ilivyokuwa desturi ya makuhani, yeye alichaguliwa kwa njia ya kupiga kura kwa kuingia ndani ya hekalu la Bwana, kusudi achome ubani. Kundi kubwa la watu walikuwa inje wakiomba saa ile Zakaria alipokuwa akichoma ubani. Halafu malaika wa Bwana akamutokea Zakaria, akisimama upande wa kuume wa mazabahu ya kuchomea ubani. Wakati Zakaria alipomwona, akahangaika na kushikwa na woga. Lakini yule malaika akamwambia: “Zakaria, usiogope, kwa maana Mungu amesikia maombi yako. Muke wako Elizabeti atakuzalia mutoto mwanaume, nawe utamwita jina lake Yoane. Utakuwa na furaha na shangwe kwa ajili yake, na watu wengi watafurahia kuzaliwa kwake, kwa maana atahesabiwa kuwa mutu mukubwa mbele ya Bwana. Hatakunywa divai wala kinywaji kikali, na atajazwa na Roho Mutakatifu tangu kuzaliwa kwake. Atawageuza Waisraeli wengi kwa kumurudilia Bwana Mungu wao. Atatangulia mbele ya kufika kwa Bwana, akiwa na roho na uwezo kama nabii Elia, kwa kuwapatanisha tena baba na watoto wao, na kuwageuza waasi wapate kuwa na hekima kama vile wenye haki. Hivi atamutayarishia Bwana watu wanaokuwa tayari kwa kumupokea.” Zakaria akamwuliza yule malaika: “Kitu gani kitakachonijulisha kwamba maneno hayo ni ya kweli? Mimi ni muzee, na muke wangu amekwisha kuzeeka sana.” Malaika akamujibu: “Mimi ni Gabrieli, anayebaki karibu na Mungu! Nimetumwa kusema nawe, kwa kukuletea habari hii njema. Maneno yale yatatimia kwa wakati wake uliopangwa, lakini kwa sababu haukuyasadiki, utakuwa bubu. Hautaweza kusema mpaka siku ile mambo hayo yatakapotimia.” Kwa muda wote watu wale walipokuwa inje, wakimungojea Zakaria, wakashangaa kwa kuona anakawia ndani ya hekalu. Alipotoka inje, hakuweza kusema nao, na watu wakatambua kwamba amepata maono ndani ya hekalu. Lakini alikuwa akifanya alama kwa mikono, kwa sababu alibaki bubu. Wakati Zakaria alipotimiza siku zake za kazi, akarudia kwenye nyumba yake. Halafu nyuma ya siku zile, muke wake Elizabeti akapata mimba. Hakutokatoka ndani ya nyumba kwa muda wa miezi mitano, akisema: “Sasa Bwana amenifanyia mema kwa kunitendea hivi; ameniondolea haya ya kutokuzaa niliyokuwa nayo mbele ya watu.” Mimba ya Elizabeti ilipotimiza miezi sita, Mungu akamutuma malaika Gabrieli katika muji mumoja wa Galilaya, unaoitwa Nazareti. Alimutuma kwa binti mumoja aliyekuwa muchumba wa mutu mumoja wa ukoo wa mufalme Daudi, aliyeitwa Yosefu. Jina la yule binti liliitwa Maria. Malaika akamufikia kwenye nyumba yao na kumwambia: “Salamu kwako, wewe uliyejaliwa neema kutoka kwa Mungu! Bwana yuko pamoja nawe.” Wakati Maria aliposikia maneno haya, akahangaika sana na kujiuliza: “Maana ya salamu hii ni nini?” Halafu malaika akamwambia: “Maria, usiogope, kwa maana Mungu amekujalia neema. Utapata mimba, utazaa mutoto mwanaume, na utamwita jina lake Yesu. Yeye atakuwa mwenye mamlaka, na ataitwa Mwana wa Mungu Mukubwa. Bwana Mungu atamuweka kuwa mutawala wa ufalme wa babu yake Daudi. Yeye atatawala taifa la Israeli hata milele, nao ufalme wake hautakuwa na mwisho.” Maria akamwuliza malaika: “Jambo hili litawezekana namna gani kwa maana mimi ningali bikira?” Malaika akamujibu: “Roho Mutakatifu atakufikia, na uwezo wa Mungu Mukubwa utakufunika kama vile kivuli. Kwa sababu hii mutoto yule atakayezaliwa ataitwa Mutakatifu na Mwana wa Mungu. Hata Elizabeti wa jamaa yako, amepata mimba, naye atazaa mutoto mwanaume, ijapokuwa yeye ni muzee. Yeye aliyekuwa akiitwa tasa, sasa huu ni mwezi wa sita wa mimba yake. Kwa maana hakuna kisichowezekana kwa Mungu.” Basi Maria akasema: “Mimi ni mujakazi wa Bwana; ifanyike kwangu sawa ulivyosema.” Kisha malaika akajiendea. Katika siku zile, Maria akafunga safari, akaenda kwa haraka katika muji mumoja uliokuwa katika vilima vya Yudea. Akafika kwenye nyumba ya Zakaria, akaingia ndani yake na kumusalimia Elizabeti. Elizabeti aliposikia salamu ya Maria, mutoto akajitingiza ndani ya tumbo lake. Elizabeti akajazwa na Roho Mutakatifu, akasema kwa sauti kubwa: “Wewe umebarikiwa kuliko wanawake wote, na mutoto utakayemuzaa amebarikiwa! Namna gani nimepata bahati hii ya kutembelewa na mama ya Bwana wangu? Kwa maana mara moja niliposikia salamu yako, mutoto akajitingiza kwa furaha ndani ya tumbo langu. Heri kwako wewe uliyesadiki kwamba maneno yale uliyoambiwa kutoka kwa Bwana yatatimizwa!” Halafu Maria akasema: “Moyo wangu unamutukuza Bwana, roho yangu inamufurahia Mungu, Mwokozi wangu; kwa maana ameniangalia kwa huruma, mimi mujakazi wake munyenyekevu. Tangu sasa watu wote wataniita mwenye heri, sababu Mungu Mwenye Uwezo, amenitendea maajabu. Jina lake ni takatifu. Yeye anawasikilia wale wanaomwogopa huruma kwa vizazi vyote. Ametenda kwa uwezo wake mukubwa, amewasambaza wale wanaofanya mipango kwa kiburi. Amewashusha wafalme wenye uwezo, lakini amewainua wanyenyekevu. Anawatajirisha wenye njaa, lakini amewaacha watajiri mikono mitupu. Amesaidia Israeli mutumishi wake, akikumbuka huruma yake, sawa alivyoahidi babu zetu, Abrahamu na wazao wake kwa milele.” Maria akakaa na Elizabeti kadiri ya miezi mitatu. Kisha akarudia kwenye nyumba yao. Wakati wa kuzaa kwa Elizabeti ulipotimia, akazaa mutoto mwanaume. Wajirani zake na wandugu zake wa jamaa waliposikia jinsi Bwana amemusikilia huruma sana, wakafurahi wote pamoja naye. Ilipotimia siku nane tangu mutoto alipozaliwa, wakaenda kumutahiri, nao wakataka kumupa jina la baba yake Zakaria. Lakini mama yake akakataa na kuwaambia kwamba jina lake litaitwa Yoane. Wakamwambia: “Mbona hakuna mutu katika jamaa yako anayeitwa kwa jina hili?” Halafu wakamwuliza baba ya mutoto kwa njia ya kufanya alama jina gani analotaka wamupe. Zakaria akaomba wamuletee kibao, naye akaandika maneno haya juu yake: “Jina lake ni Yoane.” Wote wakashangaa. Na pale pale ulimi wa Zakaria ukafunguka, akaanza tena kusema, akasifu Mungu. Basi watu wote waliokaa karibu naye wakashikwa na woga, na habari ya mambo haya yote ikaenea fasi zote katika inchi ya vilima vya Yudea. Na wote waliosikia habari ile wakafikiri juu yake na kujiuliza: “Mutoto huyu atakuwa mutu gani?” Maana hakika nguvu ya Bwana ilikuwa pamoja naye. Baba yake Zakaria akajazwa na Roho Mutakatifu, na kuanza kutabiri, akisema: “Asifiwe Bwana, Mungu wa Waisraeli, maana amewasaidia watu wake na kuwakomboa. Ametuletea Mwokozi mwenye uwezo, toka ukoo wa mutumishi wake Daudi. Ni sawa alivyosema zamani kwa njia ya manabii wake watakatifu. Aliahidi kutuokoa toka mikono ya waadui zetu, ndio wale wanaotuchukia. Aliahidi kuwasikilia babu zetu huruma; na kukumbuka agano lake takatifu, sawa alivyomwapia babu yetu Abrahamu. Alimwahidi kutuokoa toka mikono ya waadui zetu, kusudi tumutumikie pasipo woga, katika hali ya utakatifu na haki mbele yake siku zote za maisha yetu. Na wewe, mutoto wangu, utaitwa nabii wa Mungu Mukubwa, maana utatangulia mbele ya kufika kwa Bwana, kusudi umutengenezee njia. Upate kuwajulisha watu wake kwamba atawaokoa akisamehe zambi zao. Kutokana na huruma kubwa ya Mungu wetu, atatutumia mwangaza kutoka juu. Atawaangazia wale wanaoishi katika giza na wanaokaa katika kivuli cha kifo, kusudi atuongoze tupate kufuata njia ya amani.” Mutoto yule akakomaa na kuzidi kuwa na nguvu katika roho. Akakaa katika nafasi za jangwa mpaka siku alipojionyesha waziwazi mbele ya Waisraeli. Katika siku zile, Augusto, mufalme wa Roma akatoa amri kwamba wafanye hesabu ya watu wa utawala wake wote. Hesabu hii ya kwanza ilifanyika katika siku Kurenio alipokuwa liwali wa jimbo la Suria. Watu wote walienda kujiandikisha, kila mumoja katika muji wake wa kuzaliwa. Basi Yosefu naye vilevile akaondoka katika muji Nazareti, wa jimbo la Galilaya, na kwenda Yudea katika muji wa kuzaliwa wa mufalme Daudi, unaoitwa Betelehemu. Alienda kule kwa sababu alikuwa mutu wa ukoo wa Daudi. Alienda kujiandikisha kule pamoja na muchumba wake Maria ambaye alikuwa mimba. Walipokuwa kule Betelehemu, wakati wake wa kuzaa ukatimia. Akazaa mwana, ndiye muzaliwa wake wa kwanza. Akamufunika nguo za kitoto na kumulalisha katika sanduku ya kukulishia nyama, kwa sababu walikosa nafasi ya kukaa katika nyumba ya kupangisha wageni. Na katika pande zile, kulikuwa wachungaji kule katika mbuga wakichunga kondoo zao usiku. Na kwa rafla malaika wa Bwana akawatokea, na mwangaza wa utukufu wa Bwana ukawazunguka. Nao wakaogopa sana. Lakini malaika akawaambia: “Musiogope, kwa sababu ninawaletea Habari Njema itakayofurahisha sana watu wote. Leo hii Mwokozi amezaliwa kwa ajili yenu katika muji wa Daudi, yeye ndiye Kristo na Bwana. Na hiki ndicho kitambulisho kwenu: mutamukuta mutoto muchanga amefunikwa nguo za kitoto, naye amelalishwa katika sanduku ya kukulishia nyama.” Mara moja kukaonekana kundi kubwa la wamalaika kutoka mbinguni wakiwa pamoja na yule malaika, wakimutukuza Mungu na kusema: “Sifa kwa Mungu juu mbinguni, na amani katika dunia kwa watu anaowapenda.” Wale wamalaika walipoondoka na kurudia mbinguni, wachungaji wakasemezana: “Basi tuende Betelehemu, kusudi tupate kuona jambo lile lililotokea, ambalo Bwana alitujulisha.” Halafu wakaenda kwa haraka, wakawakuta Maria, Yosefu na mutoto amelalishwa katika sanduku ya kukulishia nyama. Nao walipokwisha kumwona mutoto huyo muchanga, wakaeleza maneno waliyoambiwa na malaika juu yake. Na wote waliosikia habari ile waliyoieleza wakashangaa. Lakini Maria akachunga mambo hayo yote ndani ya moyo na kuyafikiri sana. Kisha wachungaji wakarudia wakitukuza Mungu na kumusifu kwa ajili ya mambo yote waliyoyasikia na kuyaona, kwa maana yote yalifanyika sawa vile malaika alivyokuwa amewaambia. Ilipotimia siku ya kumutahiri mutoto, ndiyo siku ya nane tangu alipozaliwa, wakamupa jina lake Yesu. Jina hili ni lile malaika alilojulisha mbele mama yake hajabeba mimba. Siku zilipotimia za Maria na Yosefu kutakaswa kama vile Sheria ya Musa inavyoagiza, wakamupeleka mutoto Yerusalema, kusudi wapate kumutolea kwa Bwana. Imeandikwa katika Sheria ya Bwana: “Kila muzaliwa wa kwanza wa kiume atatolewa kwa Bwana.” Wakatoa vilevile sadaka sawa vile inavyoagizwa katika Sheria ile: “Hua wawili au vitoto viwili vya njiwa.” Wakati ule katika Yerusalema kulikuwa mutu mumoja aliyeitwa Simeoni. Mutu huyo alikuwa mwenye haki na mwenye kuogopa Mungu. Alikuwa akitazamia kwa hamu ukombozi wa taifa la Israeli. Roho Mutakatifu alikuwa pamoja naye; alikuwa amemufunulia kwamba hatakufa mbele hajamwona Kristo wa Bwana. Na ilimutokea Simeoni kuingia ndani ya hekalu, akiongozwa na Roho. Wazazi walipomuleta mutoto wao Yesu kusudi wamutendee sawa ilivyoagizwa na Sheria, Simeoni akamupokea katika mikono, akamushukuru Mungu, akisema: “Sasa, Ee Bwana, umuruhusu mutumishi wako akufe katika amani, maana umetimiza ahadi yako. Nimejionea mwenyewe wokovu unaotoka kwako, ulioutayarisha mbele ya watu wote. Ndio utakaowaangazia mataifa, na kuleta utukufu kwa watu wako Waisraeli.” Wazazi wa Yesu wakashangaa kusikia maneno yale Simeoni aliyosema juu ya mutoto. Simeoni akawabariki na kumwambia Maria, mama yake: “Mutoto huyu amezaliwa kwa sababu ya kuwaangusha na kuwasimamisha watu wengi katika Israeli. Naye atakuwa kitambulisho kutoka kwa Mungu watu watakachokipinga, kusudi mawazo ya wengi yanayofichwa yapate kufunuliwa wazi. Na kwa ngambo yako wewe, uchungu utakuchoma moyo kama upanga.” Kulikuwa vilevile nabii mumoja mwanamuke, aliyeitwa Ana, aliyekuwa binti ya Fanueli, wa kabila la Aseri. Yeye alikuwa muzee sana. Aliishi miaka saba na mume wake tangu alipoolewa. Kisha akabaki mujane, hata akaeneza umri wa miaka makumi nane na mine. Alibaki katika hekalu, akitumikia Mungu usiku na muchana, akifunga kula chakula na kuomba. Basi, akafika saa ile ile, akaanza kumushukuru Mungu. Naye akaeleza habari za mutoto huyo kwa watu wote waliokuwa wakingojea jinsi Mungu atakavyokomboa Yerusalema. Wakati wazazi wa Yesu walipokwisha kutimiza kanuni zote zilizoagizwa na Sheria ya Bwana, wakarudia pamoja naye Galilaya, katika muji wao wa Nazareti. Mutoto yule akakomaa, akazidi kuwa na nguvu, akajaa hekima, na neema ya Mungu ilikuwa pamoja naye. Kila mwaka wazazi wa Yesu walikwenda Yerusalema kuhuzuria sikukuu ya Pasaka. Yesu alipokuwa na umri wa miaka kumi na miwili, akaenda pamoja nao kule kwa sikukuu ile kama ilivyokuwa desturi. Siku za karamu zilipopita, wakarudia kwao, lakini mutoto Yesu akabaki Yerusalema bila wazazi wake kujua. Walizania kama alikuwa pamoja na wenzake aliosafiri nao. Kisha kutembea mwendo wa siku nzima, wakaanza kumutafuta katikati ya wandugu zao na ya watu waliojuana nao. Lakini kwa kuwa hawakumwona, wakarudia tena Yerusalema kumutafuta. Nyuma ya siku tatu, wakamukuta ndani ya hekalu, akiikaa katikati ya walimu wakubwa wa Sheria, akiwasikiliza na kuwauliza maulizo. Na wote waliomusikia walishangaa kuona akili yake na majibu yake. Wazazi wake walipomwona, wakashangaa sana. Mama yake akamwuliza: “Mutoto wangu, kwa nini umetufanyia kama hivi? Mimi na baba yako tulikutafuta tukiwa na wasiwasi.” Yesu akawajibu: “Kwa nini mulinitafuta? Hamujui kwamba ninapaswa kuwa katika nyumba ya Baba yangu?” Lakini hawakufahamu neno lile alilowaambia. Basi Yesu akarudia Nazareti pamoja nao, akaendelea kuwatii. Na mama yake alichunga maneno haya yote katika moyo wake. Na Yesu alizidi kuwa na hekima, na kuongezeka kimo na kuendelea kumupendeza Mungu na watu. Katika mwaka wa kumi na tano wa utawala wa Tiberio mufalme wa Roma, Pontio Pilato alikuwa liwali wa jimbo la Yudea, na Herode alikuwa mutawala wa jimbo la Galilaya na ndugu yake Filipo alikuwa mutawala wa inchi ya Iturea na ya Tarakoniti. Vilevile Lisania alikuwa mutawala wa inchi ya Abilene, nao Anasi na Kayafa walikuwa Makuhani Wakubwa. Halafu Mungu akatoa ujumbe wake kwa Yoane mwana wa Zakaria katika jangwa. Basi Yoane akapita katika inchi zote zinazokuwa pembeni ya muto Yordani, akihubiri. Akawaambia watu wageuke toka zambi zao, wabatizwe, na Mungu atawaondolea zambi. Hivi yakatimia maneno haya yaliyoandikwa katika kitabu cha maneno ya nabii Isaya: “Sauti inatangaza katika jangwa: ‘Mutengeneze njia ya Bwana, munyooshe pahali atakapopita! Hivi kila bonde litafunikwa. Kila mulima na kila kilima vitasawanishwa. Njia zenye lukumba zitanyooshwa, nazo njia zenye mashimo zitalainishwa. Kila mutu ataona jinsi Mungu atakavyotuokoa.’ ” Halafu watu wengi walimufikia Yoane kusudi awabatize. Naye aliwaambia: “Ninyi kikundi cha nyoka! Ni nani aliwaambia kwamba munaweza kuponyoka azabu ya Mungu inayokaribia? Basi muonyeshe kwa njia ya matendo kwamba mumegeuka toka zambi zenu. Musianze tu kujisemesha kwamba Abrahamu ndiye babu yenu. Ninawaambia kwamba Mungu anaweza kugeuza mawe haya kuwa watoto wa Abrahamu! Hata sasa shoka limekwisha kuwekwa tayari kwenye mashina ya miti. Kila muti usiozaa matunda mazuri utakatwa na kutupwa katika moto.” Halafu watu wale wakamwuliza: “Basi tufanye nini?” Naye akawajibu: “Mwenye kuwa na kanzu mbili atoe moja kwa yule asiyekuwa na kitu, na anayekuwa na vyakula afanye hivi vilevile.” Walipishaji wa kodi nao wakamufikia vilevile kusudi wabatizwe. Wakamwuliza: “Mwalimu, tufanye nini?” Naye akawajibu: “Musilipishe zaidi kuliko vile inavyoamuriwa.” Nao waaskari wakamwuliza: “Na sisi, tufanye nini?” Naye akawajibu: “Musifanye ukorofi kwa mutu yeyote wala kumusingizia mutu, lakini mutoshelewe na mishahara yenu.” Watu walikuwa wakitazamia kuja kwa Kristo, na wote wakazania kwamba labda Yoane ndiye yeye. Basi Yoane akawaambia wote: “Mimi ninawabatiza kwa maji, lakini yule atakayekuja nyuma yangu ni mwenye uwezo kunipita; nami sistahili hata kufungua kamba za viatu vyake. Yeye atawabatiza kwa Roho Mutakatifu na kwa moto. Anashika lungo katika mikono yake kwa kupepeta ngano. Atakusanya ngano na kuitia katika gala yake, lakini atateketeza maganda katika moto usiozimika.” Na Yoane aliwahubiria watu wale Habari Njema akiwatolea maonyo mengi mbalimbali. Yoane alimukaripia mutawala Herode juu ya kumwoa Herodia, muke wa ndugu yake Filipo na juu ya mabaya mengine. Lakini Herode akaongeza ubaya mwingine kwa kumutia Yoane ndani ya kifungo. Watu wale wote walipobatizwa, Yesu akabatizwa vilevile. Alipokuwa akiomba, mbingu zikafunguka, na Roho Mutakatifu akashuka juu yake katika hali ya kimwili kwa mufano wa njiwa. Na sauti ikasikilika toka mbinguni ikisema: “Wewe ndiwe Mwana wangu mupendwa; ninapendezwa nawe sana.” Yesu, akarudia toka kwenye muto Yordani, akijazwa na Roho, na Roho huyo akamwongoza kwenda katika jangwa. Kule akajaribiwa na Shetani kwa muda wa siku makumi ine. Kwa muda ule, yeye hakukula kitu. Na wakati siku zile zilipotimia, akasikia njaa. Halafu Shetani akamufikia na kumwambia: “Kama wewe ni Mwana wa Mungu, amuru jiwe hili ligeuke mukate.” Yesu akamujibu: “Imeandikwa katika Maandiko Matakatifu: ‘Mutu hawezi kuishi kwa mukate tu.’ ” Kisha Shetani akamupeleka kwenye nafasi inayoinuka juu sana. Akamwonyesha mara moja falme zote za dunia, na kumwambia: “Nitakupa falme hizo zote zenye uwezo na utukufu, kwa maana mimi nimezipewa zote, nami ninaweza kuzitoa kwa mutu yeyote ninayetaka. Basi ukiinama mbele yangu kwa kuniabudu, zote zitakuwa zako.” Lakini Yesu akamujibu: “Imeandikwa katika Maandiko Matakatifu: ‘Umwabudu Bwana Mungu wako na umutumikie yeye peke yake.’ ” Halafu Shetani akamupeleka Yerusalema. Akamusimamisha juu sana kwenye pembe la hekalu na kumwambia: “Kama wewe ni Mwana wa Mungu, ujitupe chini, kwa maana inaandikwa katika Maandiko Matakatifu: ‘Mungu atawaamuru wamalaika wake wakulinde. Watakubeba katika mikono yao, kusudi muguu wako usijikwae juu ya jiwe.’ ” Lakini Yesu akamujibu: “Imeandikwa katika Maandiko Matakatifu: ‘Usimujaribu Bwana Mungu wako.’ ” Shetani alipokwisha kumujaribu Yesu namna zote, akamwacha kwa muda. Yesu akarudia Galilaya akijazwa na uwezo wa Roho, na habari zake zikaenea fasi zote katika pande zile. Alifundisha katika nyumba zao za kuabudia, na kusifiwa na watu wote. Yesu akafika Nazareti, nafasi alipokomalia. Siku ya Sabato ilipotimia akaingia katika nyumba ya kuabudia kama ilivyokuwa desturi yake. Akasimama kwa kusoma Maandiko Matakatifu; wakamupa kitabu cha nabii Isaya. Halafu akakifungua na kupata nafasi inayoandikwa: “Roho wa Bwana yuko pamoja nami, maana amenichagua niwahubirie wamasikini Habari Njema. Amenituma kuwatangazia wafungwa kwamba watakombolewa nao vipofu kwamba wataona. Amenituma kuwapa wanaoteswa uhuru, na kutangaza mwaka ambao Bwana atawajalia watu neema.” Kisha akafunga kile kitabu, akakipatia mutumishi wa nyumba ya kuabudia na kuikaa. Na watu wote waliokuwa ndani ya ile nyumba ya kuabudia wakamukazia macho. Halafu akaanza kuwaambia: “Maandiko haya yametimia leo.” Nao wote wakamufurahia na kushangaa na maneno mazuri aliyosema. Wakasema: “Huyu si mwana wa Yosefu?” Yesu akawaambia: “Hakika mutaniambia fumbo hili: ‘Muganga, ujiponyeshe wewe mwenyewe!’ Na vilevile mutaniambia hivi: ‘Tumesikia mambo yote uliyotenda katika muji Kapernaumu, basi uyafanye hapa vilevile katika muji wako.’ ” Naye akaongeza kusema: “Kweli ninawaambia: hakuna nabii anayekubaliwa katika muji wake. Ninawaambia ukweli: kulikuwa wajane wengi katika inchi ya Israeli katika siku za nabii Elia. Wakati ule, mvua ilifungwa isinyeshe kwa muda wa miaka mitatu na nusu na kukakuwa njaa kubwa katika inchi yote. Lakini Elia hakutumwa kwa mutu yeyote kati yao, isipokuwa tu kwa yule mujane wa Zarepata, katika inchi ya Sidona. Vilevile kulikuwa watu wengi wenye ukoma katika Israeli katika siku za nabii Elisha, lakini hakuna mumoja kati yao aliyetakaswa, isipokuwa tu Namani wa inchi ya Suria.” Watu wote waliokuwa ndani ya ile nyumba ya kuabudia, wakakasirika sana wakati waliposikia maneno hayo. Wakasimama, wakamusukuma Yesu hata inje ya muji wao, uliojengwa juu ya kilima. Wakamupeleka kwenye maporomoko kusudi wamutupe chini. Lakini yeye akapita katikati yao, na kujiendea. Halafu Yesu akaenda Kapernaumu, katika jimbo la Galilaya. Siku ya Sabato ilipotimia, akawafundisha watu. Nao wakashangaa sana kuona namna alivyowafundisha, kwa maana aliwafundisha kama mutu mwenye mamlaka. Na ndani ya nyumba ya kuabudia kulikuwa mutu aliyeshikwa na pepo. Naye alilalamika kwa sauti kubwa, akisema: “Ee Yesu wa Nazareti, kuna maneno gani kati yako na sisi? Ulikuja kutuangamiza? Ninakutambua wewe ni nani. Wewe ni Mutakatifu wa Mungu.” Yesu akamukaripia, akimwamuru hivi: “Nyamaza, na utoke ndani ya mutu huyu!” Na yule pepo akamutupa yule mutu chini mbele ya watu, na kutoka ndani yake pasipo kumwumiza. Watu wote wakashangaa sana na kusemezana: “Hatujaona mambo kama haya! Mutu huyu anawaamuru pepo kwa mamlaka na uwezo wake, nao wanatoka!” Na habari za Yesu zikaenea katika jimbo lile lote. Yesu akatoka ndani ya ile nyumba ya kuabudia, akaenda kwa nyumba ya Simoni. Mama mukwe wa Simoni alikuwa ameshikwa na homa kali, halafu wakamwomba Yesu amuponyeshe. Basi akainama kunapokuwa yule mama, akaamuru ile homa itoke ndani yake, naye akapona. Na mara moja akasimama na kuanza kuwashugulikia. Jua lilipotua, wakamuletea Yesu watu wote wenye kuwa na magonjwa mbalimbali. Akaweka mikono yake juu ya kila mumoja wao, akawaponyesha. Pepo wakatoka ndani ya watu wengi, wakilalamika, wakisema: “Wewe ni Mwana wa Mungu!” Lakini Yesu akawakaripia, na hakuwaachilia waseme neno, kwa sababu walijua kwamba yeye ndiye Kristo. Kulipokucha kesho yake, Yesu akatoka katika muji na kwenda pahali penye ukiwa. Kundi kubwa la watu wakaanza kumutafuta. Nao walipomwona walitaka kumuzuia kusudi asitoke kwao. Lakini Yesu akawaambia: “Imenipasa kuhubiri Habari Njema ya Ufalme wa Mungu katika miji mingine vilevile, kwa maana ni kwa sababu ile nimetumwa.” Naye akaendelea kuhubiri katika Yudea ndani ya nyumba za kuabudia. Siku moja, Yesu alisimama pembeni ya ziwa la Genezareti na watu wengi walimusongasonga kusudi wasikie neno la Mungu. Akaona vyombo viwili vyenye kuezeka pembeni ya ziwa, na wavuvi walikuwa wametoka ndani yao, na walikuwa wakisafisha nyavu zao. Yesu akaingia ndani ya moja kati ya vile vyombo, nacho kilikuwa cha Simoni. Yesu akamwomba akisukume mbali kidogo na kivuko. Halafu akaikaa mule na kuwafundisha watu. Alipokwisha kufundisha, akamwambia Simoni: “Uendeshe chombo mpaka kwenye maji mengi na mushushe nyavu zenu, muvue samaki.” Simoni akajibu: “Mwalimu, tumetumika usiku kucha bila kupata kitu. Lakini kwa sababu umeniambia, nitashusha nyavu.” Na waliposhusha nyavu, wakanasa samaki wengi sana hata nyavu zao zikaanza kupasuka. Halafu wakawafanyia wale wenzao waliokuwa ndani ya chombo kingine alama kwa mikono, kusudi wakuje kuwasaidia. Wakakuja, wakajaza vyombo vyote viwili na samaki wengi, hata vyombo vikaanza kuzama. Simoni Petro alipoona mambo hayo, akapiga magoti mbele ya Yesu na kusema: “Bwana, utoke karibu nami, kwa sababu mimi ni mutu mwenye zambi!” Simoni na wote waliokuwa pamoja naye walishangaa sana kwa sababu ya wingi wa samaki waliowapata. Yakobo na Yoane wana wa Zebedayo waliokuwa wavuvi wenzake na Simoni, walishangaa vilevile. Na Yesu akamwambia Simoni: “Usiogope; tangia sasa utafanya kazi ya kuopoa watu.” Basi wakakokota vyombo vyao mpaka inchi kavu, wakaacha vyote na kumufuata. Yesu alipokuwa katika muji mumoja kati ya miji ile, kukatokea mutu aliyejaa na ukoma mwili wote. Naye alipomwona Yesu, akainama uso mpaka chini, akamusihi akisema: “Bwana, kama ukitaka, unaweza kunitakasa.” Yesu akanyoosha mukono, akamugusa na kumwambia: “Ninataka, utakaswe!” Na mara moja mutu yule akapona ukoma. Yesu akamwamuru hivi: “Usimwambie mutu neno juu ya hii. Lakini kwenda na kumwonyesha kuhani jinsi unavyokuwa sasa. Kisha utoe sadaka kama Musa alivyoamuru, kuwa ushuhuda kwa watu wote kwamba umetakaswa.” Hata hivi habari juu ya Yesu zikazidi kuvuma na makundi mengi ya watu wakakusanyika kwa kumusikiliza na kuponyeshwa magonjwa yao. Lakini alikuwa akienda mbali nao kwenye ukiwa na kuomba kule. Siku moja Yesu alipokuwa akifundisha, Wafarisayo na walimu wakubwa wa Sheria waliotoka katika kila kijiji cha jimbo la Galilaya na la Yudea na toka Yerusalema, walikuwa wakiikaa pale. Naye alikuwa akiponyesha wagonjwa kwa uwezo wa Bwana. Watu wamoja wakakuja wakimubeba mutu aliyepooza juu ya kipoyi. Wakatafuta njia ya kumwingiza ndani ya nyumba kusudi wamuweke mbele ya Yesu. Lakini kwa kuona walikosa njia ya kumwingiza ndani, kwa sababu ya wingi wa watu, wakapanda juu ya paa, wakaondosha matebura na kumushusha yule mugonjwa katikati ya watu, akiwa juu ya kipoyi chake, hata wakamufikisha mbele ya Yesu. Yesu alipoona namna walivyomwaminia, akasema: “Rafiki yangu, zambi zako zimesamehewa.” Walimu wa Sheria na Wafarisayo wakaanza kujiuliza: “Ni mutu gani huyu anayemutukana Mungu? Ni nani anayeweza kusamehe zambi, isipokuwa Mungu peke yake?” Halafu Yesu akitambua mafikiri yao, akawauliza: “Sababu gani munajiuliza mambo hayo yote? Kitu gani kinachokuwa chepesi, kusema: ‘Zambi zako zimesamehewa,’ au kusema: ‘Simama, utembee?’ Basi, ninataka mujue kwamba Mwana wa Mutu yuko na mamlaka ya kusamehe zambi hapa katika dunia.” Kwa hiyo akamwambia yule mutu aliyepooza: “Ninakuamuru, simama, utwae kipoyi chako na urudie kwako.” Pale pale mutu yule akasimama mbele yao wote, akatwaa kipoyi alichokilalia, akaenda kwake akimusifu Mungu. Wote wakashangaa na kushikwa na woga, wakamutukuza Mungu wakisema: “Leo tumeona mambo ya ajabu.” Nyuma ya mambo hayo, Yesu alipoondoka akamwona mulipishaji mumoja wa kodi anayeitwa Lawi, akiikaa katika nyumba ya kulipishia kodi. Yesu akamwambia: “Unifuate!” Lawi akasimama, akaacha vyote na kumufuata. Kisha Lawi akamufanyia Yesu karamu kubwa katika nyumba yake. Walipishaji wengi wa kodi na watu wengine walikuwa wakikula pamoja nao. Wafarisayo na walimu wa Sheria wa kikundi chao wakawanungunikia wanafunzi wake, wakisema: “Kwa sababu gani munakula na kunywa pamoja na walipishaji wa kodi na watenda mabaya?” Yesu akawajibu: “Wenye afya nzuri hawahitaji muganga, lakini wale wanaokuwa wagonjwa. Sikukuja kuwaita wenye haki, lakini wenye zambi kusudi wageuke toka zambi zao.” Watu wamoja wakamwambia Yesu: “Wanafunzi wa Yoane na wale wa Wafarisayo wanafunga mara nyingi na kuomba, lakini wanafunzi wako wanaendelea kula na kunywa.” Yesu akawajibu: “Munafikiri kwamba munaweza kuwazuiza warafiki za bwana-arusi kula chakula cha karamu wakati bwana arusi akingali pamoja nao? Hapana! Lakini kutakuwa siku bwana-arusi atakapoondoshwa kati yao. Katika siku zile ndipo watafunga kula.” Yesu akawaambia mufano huu vilevile: “Hakuna mutu anayekata kiraka kwenye nguo mupya na kukishonea juu ya nguo ya zamani. Kama anafanya vile, atakuwa amepasua ile nguo mupya na kile kiraka cha nguo mupya hakitashikamana na nguo ya zamani. Vilevile hakuna mutu anayetia divai mupya ndani ya machupa ya ngozi yenye kuzeeka. Kama akifanya vile, ile divai mupya itapasua yale machupa; divai itamwangika na machupa yatapotea bure. Lakini inafaa kutia divai mupya ndani ya machupa mapya ya ngozi. Hakuna mutu aliyekwisha kunywa divai ya zamani atakayetaka tena divai mupya. Kwa maana anasema kwamba ile ya zamani ni nzuri zaidi.” Siku moja ya Sabato, Yesu akapita katika mashamba ya ngano, wanafunzi wake wakaanza kuchumachuma masuke ya ngano, wakayasiritasirita katika mikono yao na kuyakula. Wamoja kati ya Wafarisayo wakawauliza: “Sababu gani munafanya mambo yanayokatazwa kufanya kwa siku ya Sabato?” Yesu akawajibu: “Hamujasoma bado vile Daudi alivyofanya wakati yeye mwenyewe na watu wake waliposikia njaa? Aliingia ndani ya nyumba ya Mungu, akakamata mikate mitakatifu iliyotolewa kwa Mungu, akaikula na kuwapa watu wake vilevile, ijapokuwa mikate ile iliruhusiwa kukuliwa na makuhani wenyewe tu.” Halafu Yesu akawaambia: “Mwana wa Mutu ndiye Bwana wa siku ya Sabato.” Siku ingine moja ya Sabato, Yesu akaingia katika nyumba ya kuabudia na kuanza kufundisha. Na mule ndani mulikuwa mutu mumoja mwenye kukauka mukono wa kuume. Walimu wa Sheria na Wafarisayo wakamuchunguza Yesu kusudi waone kama ataponyesha mutu kwa siku ya Sabato. Walifanya vile kusudi wapate sababu ya kumushitaki. Lakini kwa kuwa Yesu alijua mawazo yao, akamwambia yule mutu mwenye mukono unaokauka: “Simama pale mbele ya watu.” Naye akaenda kusimama pale. Kisha Yesu akawaambia: “Ninawauliza: Sheria inaturuhusu kufanya mema au mabaya kwa siku ya Sabato? Kuponyesha mutu au kumwua?” Yesu akawaangalia wote waliokuwa pale, kisha akamwambia yule mutu: “Nyoosha mukono wako.” Naye akafanya vile, na mukono wake ukakuwa muzima tena. Lakini wale wakubwa wakakasirika sana, wakaanza kusemezana wao kwa wao juu ya namna watakavyomutendea Yesu. Katika siku zile, Yesu akapanda juu ya kilima kwenda kuomba na kukesha usiku wote akiomba Mungu. Kulipokucha, akawaita wanafunzi wake, na kuchagua hawa kumi na wawili katikati yao, akawapanga jina la mitume: Simoni (Yesu aliyemupa jina la Petro) na ndugu yake Andrea, Yakobo na Yoane, Filipo na Bartolomayo, Matayo na Toma, Yakobo mwana wa Alfayo na Simoni (wa kikundi cha Wazeloti), Yuda mwana wa Yakobo na Yuda Iskariota aliyemutoa Yesu. Yesu akashuka toka kilima pamoja na wanafunzi wake, na kusimama kwenye uwanja. Pale kulikuwa wanafunzi wake pamoja na kundi kubwa sana la watu waliotoka Yerusalema, katika Yudea yote na pande za miji Tiro na Sidona pembeni ya bahari. Watu hao walikuja kumusikiliza na kuponyeshwa magonjwa yao. Na wale walioteswa na pepo waliponyeshwa. Watu wote walitaka kumugusa, kwa sababu uwezo ulikuwa ukitoka ndani yake na kuwaponyesha wote. Kisha Yesu akawaangalia wanafunzi wake na kusema: “Heri kwenu munaokuwa wamasikini, maana Ufalme wa Mungu ni kwenu. Heri kwenu munaokuwa wenye njaa sasa, maana mutashibishwa. Heri kwenu munaolia sasa, maana mutacheka. “Heri ninyi wakati watu wanapowachukia, wanapojitenga nanyi, wanapowatukana na kuchafua jina lenu kwa ajili ya Mwana wa Mutu! Mambo hayo yatakapotokea, mufurahi na kurukaruka, maana munawekewa zawadi kubwa mbinguni. Ni hivi babu zao walivyowatendea manabii. Lakini ole kwenu ninyi munaokuwa watajiri, maana hamutapata raha ingine. Ole kwenu ninyi munaoshiba sasa, maana mutasikia njaa. Ole kwenu ninyi munaocheka sasa, maana mutahuzunika na kulia. Ole kwenu ninyi wakati watu wote watakapowasifu, maana ni hivi babu zao walivyowatendea manabii wa uongo! “Lakini kwa ngambo yenu ninyi munaonisikiliza ninawaambia: muwapende waadui zenu. Muwatendee mema wale wanaowachukia. Muwaombee baraka wale wanaowalaani. Muwaombee wale wanaowaonea. Kama mutu akikupiga kofi kwa shavu moja, umugeuzie lingine vilevile. Kama mutu akikunyanganya koti yako, umwachie shemizi yako vilevile. Mutu akikuomba kitu umupe nacho, na anayekunyanganya vitu vyako, usiombe akurudishie. Muwatendee wengine sawasawa munavyotaka wawatendee ninyi vilevile. “Muko na shukrani gani kama munawapenda tu wale wanaowapenda? Kwa maana hata wenye zambi wanawapenda wale wanaowapenda. Muko na shukrani gani kama munawatendea mema tu wale wanaowatendea mema? Hata wenye zambi wanafanya hivi vilevile. Tena, muko na shukrani gani kama munawakopesha tu wale munaowatumainia kwamba watawarudishia? Hata wenye zambi wanawakopesha wenye zambi wenzao kusudi warudishiwe tena mali ile ile! Lakini muwapende waadui zenu, muwatendee mema na muwakopeshe pasipo kutumainia kurudishiwa kitu. Halafu mutapewa zawadi kubwa na mutakuwa kweli watoto wa Mungu Mukubwa kwa sababu yeye ni mwema kwa watu waovu wasiokuwa na shukrani. Mukuwe wenye huruma, kama vile Baba yenu anavyokuwa mwenye huruma. “Musiwahukumu wengine, na Mungu hatawahukumu ninyi. Musikuwe wenye kukatia wengine azabu, naye hatawaazibu ninyi. Muwasamehe wengine, na Mungu atawasamehe ninyi vilevile. Muwape wengine, na Mungu atawapa ninyi. Mutapokea kipimo kikubwa kilichojaa zaidi. Kwa maana mutapimiwa na kipimo kile munachotumia kwa wengine.” Yesu akawaambia tena wanafunzi wake mufano huu akiwauliza: “Kipofu anaweza kumwongoza kipofu mwingine? Wote wawili hawatatumbukia ndani ya shimo? Mwanafunzi hamupiti mwalimu wake akili, lakini kila mwanafunzi anayetimiza mafundisho yake, atakuwa kama mwalimu wake. “Namna gani unaona vumbi inayokuwa ndani ya jicho la ndugu yako, lakini haufikiri juu ya nguzo inayokuwa ndani ya jicho lako? Au, namna gani unaweza kumwambia ndugu yako kwamba aache umwondoe vumbi inayokuwa ndani ya jicho lake, wakati ndani ya jicho lako mungali ile nguzo. Wewe munafiki, ondosha kwanza nguzo kutoka ndani ya jicho lako, kisha utaweza kuona waziwazi na kuweza kuondosha ile vumbi inayokuwa ndani ya jicho la ndugu yako. “Hakuna muti muzuri unaoweza kutoa matunda mabaya, wala hakuna muti mubaya unaoweza kutoa matunda mazuri. Kwa maana kila muti unajulikana kwa njia ya matunda yake. Watu hawachumi matunda ya tini au mizabibu juu ya miti ya miiba. Mutu muzuri anasema maneno mazuri kutokana na uzuri wa moyo wake. Na mutu mubaya anasema maneno mabaya kutokana na ubaya wa moyo wake. Kwa maana kinywa cha mutu kinasema maneno yanayojaa ndani ya moyo wake. “Sababu gani munaniita ‘Bwana, Bwana,’ nanyi hamufanyi yale ninayowaamuru? Nitawaonyesha mufano wa mutu anayenifuata, anayesikia maneno yangu na kuyashika: anafananishwa na mutu aliyejenga nyumba, akaichimbia musingi chini sana mpaka kwenye jiwe, na kuujenga pale. Mvua kubwa iliponyesha, muto ukajaa na maji yakashambulia nyumba ile, lakini hayakuweza kuitikisa, kwa sababu ilikuwa imejengwa vizuri. Lakini yule anayesikia maneno yangu pasipo kuyashika, anafananishwa na mutu aliyejenga nyumba juu ya udongo bila kuchimba musingi. Maji kutoka muto yakaishambulia, na mara moja ikaanguka na kubomoka kabisa.” Yesu alipokwisha kusema maneno hayo yote kwa watu waliomusikiliza, akaenda Kapernaumu. Kule kulikuwa mukubwa mumoja wa waaskari aliyekuwa na mutumishi wake mupendwa sana. Mutumishi yule alikuwa mugonjwa karibu kufa. Yule mukubwa aliposikia habari ya Yesu, akatuma kwake wasimamizi wamoja wa Wayuda, kwa kumwomba akuje kumuponyesha mutumishi wake. Wale wasimamizi walipofika kwa Yesu, wakamusihi sana, wakasema: “Umufanyie mutu huyu sawa anavyokuomba, kwa maana anastahili kutendewa vile. Yeye anapenda taifa letu na ni yeye aliyetujengea nyumba yetu ya kuabudia.” Halafu Yesu akaenda pamoja nao. Alipokuwa karibu na kwa yule mukubwa wa waaskari, yule mukubwa akawatuma warafiki zake kumwambia Yesu: “Bwana, usijisumbue, kwa maana mimi sistahili kukupokea ndani ya nyumba yangu. Ndiyo sababu nilijiona kwamba sistahili kuja kwako. Lakini sema neno tu, na mutumishi wangu atapona. Hata mimi vilevile ni mutu mwenye kuwa chini ya mamlaka ya wakubwa, na tena niko na waaskari wengine wanaokuwa chini yangu. Nami nikimwambia mumoja: ‘Kwenda!’ naye anakwenda! Nikimwambia mwingine: ‘Kuja!’ naye anakuja! Nami nikimwambia mutumishi wangu: ‘Fanya hivi!’ naye anafanya vile!” Yesu aliposikia maneno haya, akashangaa sana na yule mukubwa, na kugeukia kundi la watu waliomufuata, na kusema: “Ninawaambia: katika inchi yote ya Israeli sijaona bado mutu anayekuwa na imani kubwa kama huyu.” Halafu wale wasimamizi waliotumwa wakarudia kwenye nyumba, nao wakamukuta yule mutumishi amekwisha kupona. Kesho yake nyuma ya maneno haya, Yesu akaenda katika muji Naina, nao wanafunzi wake na kundi kubwa la watu wakamufuata. Alipokaribia kwenye mulango wa ukuta wa muji, kukatokea watu wanaobeba maiti ya kijana mumoja aliyekuwa mutoto wa pekee wa mama mumoja mujane. Nao watu wengi wa muji ule walikuwa wakimusindikiza yule mama. Bwana alipomwona yule mama, akamusikilia huruma na kumwambia: “Usilie.” Kisha akajongea, akagusa sanduku, nao watu waliokuwa wakilibeba wakasimama. Akasema: “Kijana, ninakuamuru, amuka!” Halafu yule aliyekuwa maiti akaamuka, akaikaa na kuanza kusema. Na Yesu akamurudisha kwa mama yake. Watu wote wakashikwa na woga, nao wakamutukuza Mungu, wakisema: “Nabii mukubwa ametokea tena kwetu! Mungu amekuja kuwasaidia watu wake.” Na jambo hili Yesu alilolifanya likaenea katika Yudea yote na katika inchi zote zinazokuwa pembeni. Wanafunzi wa Yoane wakamwelezea mambo hayo yote yaliyotokea. Kwa hiyo Yoane akawaita wawili kati yao na kuwatuma kwa Bwana kumwuliza: “Wewe ndiwe yule aliyepaswa kuja kutuokoa au tumungojee mwingine?” Wale wanafunzi walipofika kwa Yesu wakamwambia: “Yoane Mubatizaji ametutuma kwako kukuuliza ikiwa wewe ndiwe yule aliyepaswa kuja au tumungojee mwingine.” Saa ile ile Yesu akawaponyesha watu wengi walioteswa na magonjwa na ulema mbalimbali pamoja na wenye pepo, na kuwaponyesha hata vipofu wengi. Halafu Yesu akawajibu wale wajumbe: “Mwende kumwelezea Yoane mambo muliyoona na kusikia: vipofu wanapata kuona, viwete wanatembea, wenye ukoma wanatakaswa, viziwi wanapata kusikia, wafu wanafufuliwa na Habari Njema inahubiriwa kwa wamasikini. Heri mutu yule ambaye sitakuwa kikwazo kwake.” Wale wajumbe wa Yoane walipokwisha kuondoka, Yesu akaanza kuwaambia makundi ya watu habari za Yoane akisema: “Mulienda katika jangwa kuangalia nini? Tete linalotikiswa na upepo? Hapana! Basi mulienda kuangalia nini? Mutu aliyevaa nguo nzuri? Hapana! Wale wanaovaa nguo za bei kali na kuishi katika raha wanakaa katika nyumba za kifalme. Basi mulienda kuangalia nini? Nabii? Ndiyo, ninawaambia ninyi kwamba yeye ni mukubwa kupita hata nabii. Huyu ndiye maneno haya yameandikwa juu yake katika Maandiko Matakatifu: ‘Ninamutuma mujumbe wangu akutangulie, kusudi akutengenezee njia utakayopitia!’ Ninawaambia: kati ya watu wanaoishi katika dunia, hakuna anayekuwa mukubwa kuliko Yoane. Lakini yeyote anayehesabiwa kuwa mudogo katika Ufalme wa Mungu anahesabiwa kuwa mukubwa kuliko yeye.” (Watu wote waliomusikiliza, na walipishaji wa kodi vilevile, wakakubali kwamba Mungu ni mwenye haki, hata wakabatizwa na Yoane. Lakini Wafarisayo na walimu wakubwa wa Sheria walikataa mupango wa Mungu juu yao, na kukataa kubatizwa na Yoane.) “Basi nitawafananisha watu wa kizazi hiki na nini? Wao ni watu wa namna gani? Wanafanana na watoto wanaoikaa kwenye nafasi ya makutano wanaowaita wenzao, wakisema: ‘Tuliwapigia ngoma, lakini hamukucheza! Tuliimba wimbo wa kilio, lakini hamukulia!’ Ni hivi vilevile, Yoane Mubatizaji alikuja, yeye anafunga kula chakula na kunywa divai, nanyi munasema: ‘Yuko na pepo.’ Mwana wa Mutu alikuja, yeye anakula na kunywa, nanyi munasema: ‘Angalia huyu mulafi na mulevi, rafiki ya walipishaji wa kodi na watenda maovu.’ Lakini hekima ya Mungu ilihakikishwa kuwa ya haki na wote wanaoikubali.” Siku moja Mufarisayo mumoja akamwalika Yesu kwake kuja kula chakula. Basi Yesu akaenda kwenye nyumba ya yule Mufarisayo, na kuikaa kula chakula. Katika muji ule kulikuwa mwanamuke mumoja aliyejulikana kuwa mwenye mwenendo mubaya. Mwanamuke yule alipopata habari kama Yesu alikuwa akikula ndani ya nyumba ya yule Mufarisayo, akafika akileta chupa la jiwe linalojaa marasi ya bei kali. Akakuja kuinama kwenye miguu ya Yesu, akilia. Machozi yake yakamwangika juu ya miguu ya Yesu, akaipanguza na nywele zake, akaibusu na kuipakaa marasi. Yule Mufarisayo aliyemwalika Yesu alipoona vile, akajisemesha: “Kama mutu huyu angekuwa kweli nabii, angetambua mwanamuke huyu anayemugusa ni wa namna gani. Angetambua kwamba yeye ni mwenye mwenendo mubaya.” Yesu akamwambia yule Mufarisayo: “Simoni, niko na neno la kukuuliza.” Simoni akajibu: “Mwalimu, sema.” Yesu akasema: “Kulikuwa watu wawili waliokopesha feza kutoka kwa mutu mumoja. Mumoja alikuwa na deni ya vikoroti mia tano vya feza na mwingine vikoroti makumi tano. Na kwa kuona wote wawili hawakukuwa na uwezo wa kulipa madeni yao, yule bwana akawasamehe. Sasa, uniambie, kati ya hawa wawili, ni nani atakayemupenda yule bwana zaidi?” Simoni akajibu: “Ninazani kwamba ni yule aliyesamehewa deni kubwa zaidi.” Na Yesu akamwambia: “Umejibu vizuri.” Halafu akamugeukia yule mwanamuke na kumwambia Simoni: “Unamwona mwanamuke huyu? Niliingia ndani ya nyumba yako, nawe haukunipa maji ya kunawa miguu yangu, lakini mwanamuke huyu amenawa miguu yangu na machozi yake na kuipanguza na nywele zake. Wewe haukunibusu kwa kunisalimia, lakini mwanamuke huyu hakuacha kubusu miguu yangu tangu nilipoingia humu. Wewe haukupakaa mafuta juu ya kichwa changu, lakini yeye amepakaa marasi juu ya miguu yangu. Ni kwa sababu hii ninakuambia kwamba upendo ambao mwanamuke huyu alioonyesha unahakikisha kwamba Mungu amemusamehe zambi zake zinazokuwa nyingi. Lakini yule anayesamehewa kwa machache haonyeshi upendo zaidi.” Kisha Yesu akamwambia yule mwanamuke: “Zambi zako zimesamehewa.” Na waalikwa wengine waliokuwa wakikula pamoja na Yesu, wakaanza kujisemesha: “Ni mutu gani huyu anayesamehe zambi?” Lakini Yesu akamwambia tena yule mwanamuke: “Kwenda na amani, imani yako imekuokoa.” Nyuma ya pale Yesu akapita katika miji na vijiji mbalimbali, akihubiri na kutangaza Habari Njema ya Ufalme wa Mungu. Wale wanafunzi wake kumi na wawili walienda naye pamoja na wanawake wamoja ambao alikuwa ameondosha pepo ndani yao na magonjwa mengine. Kati ya wale wanawake kulikuwa Maria (aliyeitwa wa Magdala), aliyekuwa ameponyeshwa pepo saba; na Yoana muke wa Kuza, huyo mume wake alikuwa musimamizi wa mali ya Herode, pamoja na Suzana na wengine wengi. Wanawake hawa walitumia mali yao kwa kuwasaidia Yesu na wanafunzi wake. Watu walikuwa wakimufikia Yesu toka miji mbalimbali, na kundi kubwa la watu walikusanyika. Halafu akawaambia mufano huu: “Mupandaji mumoja alikwenda kupanda mbegu. Alipokuwa akipanda mbegu katika shamba lake, zimoja zikaanguka pembeni ya njia. Watu wakazikanyagakanyaga na ndege wakazikula. Zingine zikaanguka kwenye udongo wenye mawe. Nazo zilipoota, mara moja zikakauka kwa sababu ya ukosefu wa maji. Mbegu zingine zikaanguka katikati ya miiba. Ile miiba ikaota pamoja na mbegu, na kuzisonga. Lakini mbegu zingine zikaanguka katika udongo muzuri; nazo zikaota na kutoa matunda, kila moja punje mia.” Yesu alipokwisha kuwaambia hayo yote, akasema: “Mwenye kuwa na masikio ya kusikia, asikie!” Halafu wanafunzi wa Yesu wakamwuliza maana ya mufano huo. Akawajibu: “Ninyi mumefunuliwa kujua siri ya Ufalme wa Mungu, lakini kwa watu wengine si vile. Wao wanaambiwa maneno hayo kwa njia ya mifano, kusudi waangalie, lakini wasione kitu, nao wasikie, lakini wasifahamu kitu.” “Basi hii ndiyo maana ya ule mufano wa mupandaji: mbegu ni mufano wa neno la Mungu. Nafasi ile mbegu zilipoanguka pembeni ya njia ni mufano wa watu wanaosikia neno la Mungu. Lakini Shetani anakuja na kuondoa lile neno katika mioyo yao kusudi wasiamini na kuokolewa. Udongo wenye mawe pahali mbegu zilipoanguka ni mufano wa watu wanaosikia neno na kulipokea kwa furaha, lakini halizami ndani yao kama mizizi. Wanaliaminia kwa muda mufupi tu, nayo majaribu yanapowafikia, wanaliacha. Na mbegu zilizoanguka katika miiba ni mufano wa wale wanaosikia, lakini masumbuko, utajiri na raha ya dunia vinawasonga hata wanashindwa kutoa matunda yanayokomaa. Nao udongo muzuri walimopanda mbegu, ni mufano wa watu wanaosikia neno la Mungu na kulishika kwa moyo mwema na kwa uhaki. Ndio wale wanaovumulia hata wanatoa matunda mazuri. “Hakuna mutu anayewakisha taa na kuifunika na chombo fulani au kuiweka chini ya kitanda. Lakini anaiweka juu ya kinara kusudi wanaoingia ndani wapate kuona mwangaza. Na ni hivi hakuna chochote kinachofichwa kitakachokosa kuonekana wazi, wala hakuna siri itakayokosa kufunuliwa waziwazi. “Basi mufanye angalisho na jinsi munavyosikia maneno. Kwa maana mutu anayekuwa na kitu, ataongezewa kingine, lakini mutu asiyekuwa na kitu, atanyanganywa kile anachozania kuwa nacho.” Mama na wandugu za Yesu wakakuja kumwona, lakini hawakuweza kufika karibu naye kwa ajili ya kundi kubwa la watu. Halafu watu wakamwambia Yesu: “Mama yako na wandugu zako wanasimama inje, wanataka kukuona.” Lakini Yesu akawajibu: “Mama yangu na wandugu zangu ni wale wanaosikia neno la Mungu na kulishika.” Siku moja Yesu akaingia ndani ya chombo pamoja na wanafunzi wake. Naye akawaambia: “Tuvuke ngambo ya ziwa.” Basi wakaondoka. Nao walipokuwa wakivuka ziwa, Yesu akalala usingizi. Mara moja zoruba kali ikaanza kuvuma, hata maji yakaanza kuingia ndani ya chombo, nao wakakuwa katika hatari. Basi wanafunzi wake wakamujongelea, wakamwamusha wakisema: “Bwana, Bwana, tunakufa!” Yesu alipoamuka, akakaripia zoruba, nayo ikakoma na maji yakatulia. Halafu akawaambia wanafunzi wake: “Imani yenu iko wapi?” Nao wakaogopa na kushangaa, wakiulizana: “Huyu ni mutu gani? Anaamuru hata zoruba na ziwa, navyo vinamutii!” Yesu na wanafunzi wake wakaezeka chombo katika inchi ya Wagerasi, kuelekea Galilaya. Yesu alipotoka ndani ya chombo, akakutana na mutu mumoja kule katika muji aliyeshikwa na pepo. Mutu yule hakuvaa nguo tangu siku nyingi, wala hakuishi ndani ya nyumba, lakini aliishi kwenye makaburi. Wakati alipomwona Yesu, akalalamika na kuanguka mbele yake, na kusema kwa nguvu: “Yesu, Mwana wa Mungu Mukubwa, kuna neno kati yako na mimi? Ninakusihi, usinitese!” Alisema vile kwa sababu Yesu alikuwa amemwamuru huyo pepo, atoke ndani ya yule mutu. Huyo pepo alimukamata mutu yule mara nyingi, na ijapokuwa watu walimufunga na minyororo na vifungo vya chuma kusudi asitoroke, yeye alivikata. Na yule pepo alimusukuma kwenda katika jangwa. Yesu akamwuliza: “Jina lako nani?” Naye akamujibu: “Jina langu ni ‘Jeshi.’ ” Alisema vile kwa sababu ndani ya mutu yule mulikuwa pepo wengi. Nao wale pepo walimusihi Yesu kwamba atakapowafukuza asiwaamuru kutumbukia ndani ya shimo lisilokuwa na mwisho. Na karibu na pale kulikuwa kundi la nguruwe wengi waliokuwa wakijitafutia chakula kwenye mulima. Wale pepo wakamusihi Yesu awaruhusu kuingia ndani ya wale nguruwe. Naye akawaruhusu. Basi pepo wakamutoka mutu yule na kuingia ndani ya wale nguruwe. Kundi zima la nguruwe wakatelemuka mbio kwenye mulima na kutumbukia ndani ya maji, nao wakazama. Wachungaji wa nguruwe walipoona jambo lililotokea, wakaenda mbio kupasha habari katika muji na katika vijiji. Watu wakakuja kusudi waone jambo lile. Walipofika kwa Yesu, wakamukuta yule mutu aliyetokwa na pepo akiikaa mbele ya Yesu, akiwa amevaa nguo, nayo akili yake ikiwa sawa. Basi watu wale wakaogopa. Wale walioona yale yaliyotendeka wakawaelezea watu namna yule aliyekuwa na pepo alivyoponyeshwa. Halafu watu wote wa inchi ya Wagerasi wakashikwa na woga mukubwa, kwa hiyo wakamwomba Yesu aondoke kwao. Basi Yesu akaingia ndani ya chombo, kusudi apate kuondoka kule. Mutu yule aliyeponyeshwa pepo akamusihi Yesu aende pamoja naye, lakini akamukatalia, akimwambia: “Rudia kwako na ueleze mambo yote Mungu aliyokutendea.” Basi yule mutu akajiendea, na kutangaza fasi zote katika muji wake mambo Yesu aliyomutendea. Yesu alipovuka kurudia ngambo ingine ya ziwa, watu wengi wakamupokea kwa furaha, kwa sababu wote walikuwa wakimungojea. Mukubwa mumoja wa nyumba ya kuabudia aliyeitwa Yairo akafika. Alijitupa mbele ya Yesu na kumusihi afike kwake, kwa sababu alikuwa na mutoto mumoja binti wa pekee mwenye umri wa miaka yapata kumi na miwili, na aliyekuwa karibu kufa. Yesu alipokuwa akienda kule, kundi kubwa la watu walimusongasonga. Kati yao kulikuwa mwanamuke mumoja mwenye ugonjwa wa kutokwa na damu kwa muda wa miaka kumi na miwili. Alikuwa ametumia mali yake yote kwa kulipa waganga, lakini hakuna hata mumoja wao ambaye aliweza kumuponyesha. Mwanamuke huyu akakuja nyuma ya Yesu na kugusa upindo wa nguo yake. Na mara moja akapona ule ugonjwa wa kutokwa na damu. Yesu akauliza: “Ni nani aliyenigusa?” Watu wote wakakana, lakini Petro akasema: “Bwana, hauoni kwamba watu wengi wanakuzunguka na kukusonga?” Lakini Yesu akasema: “Kuna mutu aliyenigusa kwa maana nimejisikia kwamba nguvu zimenitoka.” Yule mwanamuke alipoona kwamba ametambulikana, akakuja akitetemeka kwa woga na kujitupa mbele ya Yesu. Na pale mbele ya watu wote, akaeleza sababu gani alimugusa na namna alivyoponyeshwa mara moja. Na Yesu akamwambia: “Binti yangu, imani yako imekuponyesha. Ujiendee na amani.” Yesu alipokuwa hajamaliza kusema maneno hayo, mujumbe mumoja akafika toka kwa yule mukubwa Yairo wa nyumba ya kuabudia na kumwambia: “Binti yako amekwisha kufa. Usiendelee kumusumbua Mwalimu.” Lakini Yesu aliposikia vile, akamwambia Yairo: “Usiogope, amini tu, atapona.” Yesu alipofika ndani ya nyumba ya Yairo, hakuruhusu mutu kuingia pamoja naye isipokuwa Petro, Yoane, Yakobo, baba na mama wa mutoto. Watu wote walikuwa wakilia na kusikitika sana kwa ajili ya kifo cha mutoto. Lakini Yesu akasema: “Musilie, kwa maana hakufi, lakini analala tu!” Nao wakamuchekelea kwa sababu walijua kwamba amekwisha kufa. Lakini Yesu akamushika mukono na kumwambia kwa sauti kubwa: “Mutoto, simama!” Naye akakuwa tena muzima, na mara moja akasimama. Yesu akawaamuru wamupe chakula. Wazazi wake wakashangaa sana na Yesu akawaagiza wasimwambie mutu yeyote yale yaliyotokea. Yesu akawakusanya wanafunzi wake kumi na wawili na kuwapatia uwezo na mamlaka ya kufukuza pepo, na uwezo wa kuponyesha wagonjwa. Halafu akawatuma kuhubiri habari za Ufalme wa Mungu na kuwaponyesha wagonjwa, akiwaagiza: “Musibebe kitu chochote kwa safari yenu, hata ikiwa fimbo, mufuko, mukate wala feza na hata mumoja wenu asivae kanzu mbili. Na nafasi yoyote watakapowakaribisha ndani ya nyumba mubakie mule mpaka mutakapotoka kule. Na katika muji wowote watu watakapokataa kuwakaribisha, mutoke kule na mukungute mavumbi toka juu ya miguu yenu. Jambo hili litakuwa ushuhuda juu yao.” Basi wanafunzi wakaondoka, wakapita katika vijiji mbalimbali, wakihubiri Habari Njema na kuponyesha watu kila fasi. Liwali Herode akasikia habari za mambo yote yaliyofanyika. Kwa hiyo akafazaika kwa sababu watu wamoja walikuwa wakisema kwamba Yoane Mubatizaji amefufuka. Na wengine walikuwa wakisema kwamba Elia ametokea. Na wengine walisema kwamba mumoja wa manabii wa zamani amefufuka. Lakini Herode alisema: “Mimi nimeamuru Yoane akatwe kichwa. Basi huyu ninayesikia habari zake ni nani?” Naye akatafuta namna ya kumwona Yesu. Mitume waliporudia toka kuhubiri wakamwelezea Yesu mambo yote waliyofanya. Kisha akaondoka pamoja nao na kwenda kwenye nafasi ya upekee karibu na muji Betesaida. Lakini makundi ya watu walipopata habari ile, wakamufuata mpaka kule. Yesu akawapokea na kuanza kusema nao juu ya Ufalme wa Mungu, na vilevile akawaponyesha wale waliohitaji kuponyeshwa. Jua lilipoanza kushuka, wanafunzi kumi na wawili wa Yesu wakamufikia na kumwambia: “Hapa tunapokuwa ni katika pori. Uage makundi haya ya watu kusudi waende katika vijiji vinavyokuwa hapa karibu na kwenye nyumba kule katika mbuga kwa kujitafutia chakula na nafasi ya kulala.” Lakini Yesu akawajibu: “Ninyi wenyewe muwape chakula!” Nao wakajibu: “Sisi tuko tu na mikate mitano na samaki mbili. Unataka sisi wenyewe tuende kuwanunulia watu hawa wote chakula?” (Watu waliokuwa pale walikuwa yapata wanaume elfu tano.) Yesu akawaamuru wanafunzi wake wawaikalishe kwa makundi ya watu makumi tano tano. Nao wanafunzi wakafanya vile, wakawaikalisha watu wote. Kisha Yesu akatwaa ile mikate mitano na samaki mbili, akainua macho mbinguni, akamushukuru Mungu. Halafu akaimega, akawapa wanafunzi waigawanyie watu. Wote wakakula na kushiba. Nao wanafunzi wakaokota vipande vilivyobaki, wakajaza vitunga kumi na viwili. Siku moja Yesu alipokuwa akiomba kwenye nafasi ya upekee, nao wanafunzi wake wakiwa pale karibu naye, akawauliza: “Watu wanasema kwamba mimi ni nani?” Nao wakajibu: “Wamoja wanasema kwamba wewe ni Yoane Mubatizaji, wengine wanasema kwamba wewe ni Elia, na wengine wanasema kwamba wewe ni mumoja wa manabii wa zamani aliyefufuka.” Na halafu Yesu akawauliza: “Na ninyi munasema kwamba mimi ni nani?” Petro akamujibu: “Wewe ni Masiya wa Mungu.” Halafu Yesu akawaagiza wanafunzi wake kwa nguvu wasimwambie mutu yeyote maneno hayo. Naye akaongeza kuwaambia: “Sherti Mwana wa Mutu ateswe na kukataliwa na wasimamizi wa watu, pamoja na walimu wa Sheria. Atauawa na kwa siku ya tatu kisha kufa kwake, atafufuka.” Kisha akawaambia wote: “Kama mutu akitaka kunifuata, asijishugulikie mwenyewe, lakini ajitolee kwa kubeba musalaba wake kila siku na kunifuata. Kwa maana mutu anayetaka kulinda uzima wake ataupoteza; lakini yule atakayetoa uzima wake kwa ajili yangu ataulinda. Ni faida gani kwa mutu kupata utajiri wote wa dunia, lakini anapoteza uzima wake mwenyewe au kujiangamiza? Kwa hiyo mutu yeyote anayesikia haya juu yangu na juu ya mafundisho yangu, Mwana wa Mutu atasikia haya juu yake vilevile. Itakuwa vile atakapokuja katika utukufu wake, akitukuzwa na Baba yake pamoja na wamalaika wake watakatifu. Kweli ninawaambia: wamoja kati ya watu wanaokuwa hapa hawatakufa mbele ya kuona Ufalme wa Mungu unasimama.” Ilipotimia karibu siku nane nyuma ya pale Yesu aliposema maneno hayo, yeye akawatwaa Petro, Yakobo na Yoane, akapanda pamoja nao kwa mulima kwa kuomba. Naye alipokuwa akiomba, sura yake ikageuka, nazo nguo zake zikageuka nyeupe sana na zenye kumetameta. Kwa wakati ule Petro na wenzake walikuwa wamewezwa sana na usingizi; lakini wakaamuka, wakaona ule utukufu wa Yesu na wale watu wawili waliokuwa wakisimama pamoja naye. Watu wale walipokuwa wakiachana na Yesu, Petro akamwambia: “Bwana, ni vizuri kuona sisi tuko hapa. Tujenge vibanda vitatu, kimoja chako, kimoja cha Musa na kingine cha Elia.” (Naye alisema hayo bila kufikiri.) Alipokuwa hajamaliza kusema, wingu likatokea na kuwafunika. Nao wanafunzi wale wakaogopa kwa kuona wamefunikwa na lile wingu. Na sauti ikasikilika toka katikati ya lile wingu, ikisema: “Huyu ni Mwana wangu niliyemuchagua. Mumusikilize!” Nyuma ya kusikilika kwa sauti ile, Yesu akaonekana amebaki peke yake. Wale wanafunzi wakachunga mambo hayo yote kwa siri wala hawakumwambia mutu neno katika siku zile. Kesho yake, Yesu na wale wanafunzi watatu waliposhuka toka kwa mulima, kundi kubwa la watu wakamufikia. Na mutu mumoja kati ya kundi akalalamika, akisema: “Mwalimu, ninakusihi umwangalie mwana wangu, kwa maana yeye ni mutoto wa pekee! Pepo anapomukamata, mara moja mutoto analalamika, na yule pepo anamutikisatikisa kwa nguvu hata pofu inamutoka. Huyo pepo hatoki ndani yake upesi, naye anamutesa sana. Niliwasihi wanafunzi wako wamufukuze, lakini hawakuweza.” Na Yesu akajibu: “Ee ninyi watu wa kizazi kisichoamini Mungu na chenye kupotoka! Nitakaa pamoja nanyi tena mpaka wakati gani? Nitawavumilia tena mpaka wakati gani? Umulete mutoto wako hapa.” Yule mutoto alipokuwa akijongea karibu na Yesu, yule pepo akamutupa chini na kumutikisa kwa nguvu. Lakini Yesu akamukaripia yule pepo na kumuponyesha mutoto. Kisha akamurudisha kwa baba yake. Na watu wote wakashangaa sana kwa kuona uwezo mukubwa wa Mungu. Nao wote walipokuwa wakishangaa juu ya mambo hayo yote Yesu aliyofanya, yeye akawaambia wanafunzi wake: “Munitegee sikio vizuri: Mwana wa Mutu atatolewa katika mikono ya watu.” Lakini wao hawakufahamu maana ya maneno hayo, kwa sababu yalikuwa yamefichwa kwao, kusudi wasipate kuyatambua. Nao waliogopa kumwuliza maana yake. Wanafunzi waliingiwa na wazo la kutafuta kujua nani anayekuwa mukubwa kati yao. Yesu akatambua mawazo yao. Kwa hiyo akatwaa mutoto akamuweka karibu naye na kuwaambia: “Anayemupokea mutoto mudogo kama huyu kwa jina langu, ananipokea mimi. Naye anayenipokea mimi, anamupokea yule aliyenituma. Kwa maana yule anayekuwa mudogo kati yenu ndiye anayekuwa mukubwa.” Naye Yoane akasema: “Bwana, tulimwona mutu mumoja akifukuza pepo kwa jina lako, nasi tulimukataza, kwa sababu yeye si wa kundi letu.” Lakini Yesu akamujibu: “Musimukataze, kwa maana yule asiyekuwa adui yenu ni wa upande wenu.” Siku za Yesu za kunyanyuliwa mbinguni zikakaribia. Kwa hiyo akakusudia sana kwenda Yerusalema, akawatuma wajumbe watangulie mbele yake. Wale wajumbe wakaondoka na kuingia katika kijiji kimoja cha Wasamaria kusudi wamutayarishie vitu vyote kule. Lakini wale wakaaji wakakataa kumupokea Yesu kwao kwa sababu alikuwa katika safari kwenda Yerusalema. Wanafunzi wake, Yakobo na Yoane walipoona mambo hayo, wakasema: “Bwana, unataka tuombe moto uwashukie toka mbinguni na kuwateketeza?” Lakini Yesu akawageukia na kuwakaripia. Kisha wakaondoka kwenda katika kijiji kingine. Nao walipokuwa katika njia, mutu mumoja akamwambia Yesu: “Nitakufuata popote utakapokwenda.” Yesu akamwambia: “Mbweha wako na makao yao ndani ya matundu nao ndege wako na chicha, lakini Mwana wa Mutu hana nafasi ya kulala.” Naye Yesu akamwambia mutu mwingine: “Unifuate.” Lakini mutu yule akamujibu: “Bwana, unipe ruhusa niende kwanza kuzika baba yangu.” Yesu akamwambia: “Uwaache hao wafu wazike wafu wao, lakini wewe uende kutangaza habari ya Ufalme wa Mungu.” Mutu mwingine akasema: “Bwana, nitakufuata lakini unipe ruhusa niende kwanza kuaga jamaa yangu.” Lakini Yesu akamujibu: “Mutu yeyote anayeanza kulima na kuanza tena kuangalia nyuma hafai kutumika katika Ufalme wa Mungu.” Nyuma ya maneno hayo, Bwana akawachagua watu wengine makumi saba. Naye akawatuma wawili wawili wamutangulie kupita katika kila muji na kila nafasi yeye mwenyewe alipokuwa amekusudia kwenda. Akawaambia: “Mavuno ni mengi, lakini watumishi ni wachache. Basi muombe Bwana wa mavuno atume watumishi kwa kuyavuna. Muende! Muangalie, ninawatuma kama wana-kondoo katikati ya imbwa wa pori. Musibebe feza, wala mufuko, wala viatu, na musimusalimie mutu katika njia. Na katika nyumba yoyote mutakapoingia, mutoe kwanza salamu mukisema: ‘Amani ikuwe katika nyumba hii!’ Kama mule mukiwa mutu anayekuwa tayari kupokea amani, atakaa na amani ile muliyomutakia. Kama si vile, amani ile itawarudilia. Mukae ndani ya nyumba ile, nanyi mukule na kunywa chochote watakachowapa, kwa maana mutumishi anastahili kupewa mushahara wake. Musihame nyumba kwa nyumba. Na katika muji wowote mutakamoingia, watu wakiwakaribisha, mukule na kunywa kile watakachowapa. Muponyeshe wagonjwa wanaokuwa mule na kuwaambia wakaaji: ‘Ufalme wa Mungu umewakaribia ninyi.’ Lakini katika muji wowote mutakamoingia, nao wakaaji wake wasipowakaribisha, muende kwenye viwanja vyake vya makutano na kusema: ‘Tunawakungutia ninyi hata mavumbi ya muji wenu toka juu ya miguu yetu kuwa ushuhuda juu yenu. Na hata hivi mujue vizuri kwamba Ufalme wa Mungu umewakaribia.’ Ninawaambia hakika kwamba kwa Siku ya hukumu muji ule utaazibiwa vikali zaidi kuliko muji Sodoma.” Yesu akaendelea kusema: “Ole kwako muji Korazini! Ole kwako muji Betesaida! Kwa maana kama miujiza iliyofanyika ndani yenu ingefanyika katika muji wa Tiro na wa Sidona, wakaaji wa kule wangekwisha zamani kuonyesha masikitiko yao kwa kuvaa magunia na kujipakaa majivu, na kugeuka toka zambi zao. Kwa hiyo, Siku ile ya hukumu, mutaazibiwa vikali zaidi kuliko Tiro na Sidona. Nawe muji Kapernaumu, unafikiri kwamba utapandishwa mpaka mbinguni? Utashushwa mpaka chini katika kuzimu.” Yesu akaongeza kuwaambia wanafunzi wake: “Yule anayewasikiliza ninyi, ananisikiliza mimi; yule asiyewapokea ninyi, hanipokei mimi, na yule asiyenipokea mimi, hamupokei yule aliyenituma.” Wale wanafunzi makumi saba wakarudia wakijazwa na furaha, nao wakasema: “Bwana, hata pepo wanatutii tunapowaamuru kwa jina lako!” Naye Yesu akamwambia: “Nilimwona Shetani akianguka kama umeme toka mbinguni. Muangalie, nimewapa uwezo wa kukanyaga nyoka na nge na mamlaka ya kumushinda yule adui Shetani; wala hakuna kitu chochote kitakachowazuru. Hata hivi musifurahi kwa sababu pepo wanawatii, lakini mufurahi kwa sababu majina yenu yameandikwa mbinguni.” Saa ile ile, Yesu akajazwa na furaha kwa uwezo wa Roho Mutakatifu, naye akasema: “Ee Baba, Bwana wa mbingu na dunia, ninakushukuru kwa maana mambo uliyoyaficha kwa watu wenye hekima na elimu, umeyafunua kwa wanaokuwa wadogo. Ndiyo Baba, hayo yote ni kutokana na mapenzi yako. “Baba yangu, umeweka vitu vyote katika mikono yangu. Hakuna mutu anayemujua Mwana isipokuwa Baba, wala hakuna anayemujua Baba isipokuwa Mwana na yeyote ambaye Mwana anataka kumujulisha kwake.” Kisha Yesu akawageukia wanafunzi wake wakiwa peke yao, akawaambia: “Heri watu wanaoona mambo yale munayoona! Kwa maana ninawaambia: manabii wengi na wafalme walitamani kuona mambo munayoyaona, lakini hawakuyaona, na kusikia maneno munayoyasikia, lakini hawakuyasikia.” Halafu mwalimu mumoja wa Sheria akasimama na kumwuliza Yesu kwa kumupima: “Mwalimu, nifanye nini kusudi nipate uzima wa milele?” Yesu akamujibu: “Imeandikwa namna gani katika Sheria? Unaielewa namna gani unapoisoma?” Mutu yule akamujibu kwa maneno haya: “ ‘Umupende Bwana Mungu wako kwa moyo wako wote, kwa roho yako yote, kwa nguvu yako yote na kwa akili yako yote.’ Vilevile, ‘Umupende mwenzako kama vile unavyojipenda mwenyewe.’ ” Basi Yesu akamwambia: “Umejibu vizuri. Fanya sawa vile unavyosema, nawe utaishi milele.” Lakini kwa kutaka kujipatia haki, yeye akamwuliza Yesu: “Mwenzangu ni nani?” Yesu akajibu akimwelezea: “Mutu mumoja alitoka Yerusalema akishuka kwenda Yeriko. Alipokuwa katika njia, akashambuliwa na wanyanganyi, wakamuvua nguo, wakamupigapiga, wakajiendea, wakimwacha karibu kufa. Kukatokea kuhani mumoja akishuka katika njia ile ile. Wakati alipomwona yule mutu, akapita pembeni na kujiendea. Vilevile Mulawi mumoja akafika kwenye nafasi ile, naye alipomwona mutu yule, akapita pembeni na kujiendea. Lakini Musamaria mumoja, alikuwa akisafiri vilevile katika njia ile, akafika kwenye nafasi ile yule mutu alipokuwa. Wakati alipomwona, akamusikilia huruma. Akajongea karibu naye, akamutunza vidonda, akivimwangia divai na kuvimimia mafuta na kuvifunga na vitambaa. Kisha akamupandisha juu ya punda wake, na kumupeleka kwenye nyumba ya kupangisha wageni na kumuchunga. Kesho yake akatwaa vikoroti viwili vya feza, na kuvitoa kwa mwenye nyumba, akimwambia: ‘Umuchunge mutu huyu, na feza zingine utakazotumia zaidi ya hizi kwa matunzo yake, nitazilipa kwako nitakaporudia.’ ” Halafu Yesu akamwuliza yule mwalimu wa Sheria: “Kati ya hawa watatu ni nani aliyemutendea yule mutu aliyeshambuliwa na wanyanganyi kama vile mwenzake?” Naye akajibu: “Ni yule aliyemusikilia huruma.” Halafu Yesu akamwambia: “Kwenda, nawe ufanye sawa sawa.” Yesu na wanafunzi wake walipokuwa wakisafiri, wakaingia katika kijiji kimoja. Kule mwanamuke mumoja aliyeitwa Marta akamukaribisha ndani ya nyumba yake. Marta alikuwa na dada yake mudogo aliyeitwa Maria. Huyo aliikaa mbele ya Bwana, akisikiliza mafundisho yake. Lakini Marta alikuwa anafungwa na kazi nyingi za nyumba. Kwa hiyo akamwendea Yesu na kumwambia: “Bwana, haikuhangaishi kitu kuona jinsi dada yangu anavyoniachilia kutumika mimi peke? Umwambie anisaidie.” Bwana akamujibu: “Marta! Marta! Kwa nini unahangaika na kusumbuka kwa ajili ya vitu vingi? Kuna kitu kimoja tu cha lazima. Maria amechagua kitu kinachokuwa kizuri zaidi ambacho hakuna mutu atakayekiondoa kwake.” Ilikuwa siku moja, Yesu alikuwa nafasi fulani akiomba. Alipomaliza kuomba, mumoja kati ya wanafunzi wake akamwambia: “Bwana, utufundishe kuomba, kama vile Yoane alivyowafundisha wanafunzi wake.” Yesu akawaambia: “Munapoomba, museme: ‘Baba! Jina lako litukuzwe; Ufalme wako ukuje. Utupe chakula chetu cha kila siku. Utusamehe zambi zetu, maana sisi vilevile tunawasamehe wote wanaotukosea, usituache kuingia katika majaribu.’ ” Kisha Yesu akawaambia wanafunzi wake: “Kwa mufano, mumoja kati yenu yuko na rafiki, naye anamwendea katikati ya usiku kwa kumwambia: ‘Rafiki yangu, ninakuomba unikopeshe mikate mitatu, kwa maana mumoja kati ya warafiki zangu amenifikia kutoka safari, nami sina chakula cha kumupatia.’ Na yule anayekuwa ndani ya nyumba akimujibu: ‘Usiniuzi! Mulango umekwisha kufungwa. Mimi na watoto wangu tumekwisha kulala; siwezi kuamuka kwa kukupatia mikate.’ Hakika ninawaambia kwamba hataamuka kumupatia mikate kwa sababu yeye ni rafiki yake tu, lakini sababu ya kusihi sana kwa rafiki yake, ataamuka na kumupatia vyote anavyohitaji. Nami ninawaambia: muombe nanyi mutapewa; mutafute nanyi mutapata; mupige hodi nanyi mutafunguliwa mulango. Kwa maana kila mutu anayeomba anapewa; anayetafuta anapata, anayepiga hodi anafunguliwa mulango. Ni baba gani kati yenu anaweza kumupa mutoto wake nyoka kama akimwomba samaki? Au anayeweza kumupa nge kama akimwomba yai? Basi ikiwa ninyi munaokuwa waovu munajua kuwapa watoto wenu vitu vizuri, inaonyesha hakika kwamba Baba yenu anayekuwa mbinguni atawapa Roho Mutakatifu wale wanaomwomba kwake.” Yesu alikuwa akifukuza pepo aliyemufanya mutu mumoja kuwa bubu. Yule pepo alipotoka, yule bubu akaanza kusema. Na makundi ya watu wakashangaa sana. Lakini wamoja kati yao wakasema: “Anafukuza pepo kwa uwezo wa Belzebuli, yule mukubwa wa pepo.” Na wengine walitaka kumupima wakimwomba awaonyeshe kitambulisho kinachohakikisha kwamba uwezo wake umetoka kwa Mungu. Lakini yeye akiwa anatambua mawazo yao, akawaambia: “Watu wa ufalme wowote wakigombana wao kwa wao, ufalme ule utaanguka. Na watu wa jamaa moja wakigombana wao kwa wao, jamaa ile itaanguka. Basi ikiwa Shetani akijigombanisha mwenyewe, ufalme wake hautadumu. Ninasema hivi, kwa maana ninyi munasema kama ninafukuza pepo kwa uwezo wa Belzebuli. Tena ikiwa ninafukuza pepo kwa uwezo wa Belzebuli, basi watu wa kikundi chenu wanawafukuza kwa uwezo wa nani? Watu hao watashuhudia kwa njia ya matendo yao kwamba ninyi ni wakosaji. Kwa ngambo yangu, ikiwa mimi ninafukuza pepo kwa uwezo wa Mungu, hii inaonyesha kwamba Ufalme wa Mungu umekwisha kufika kati yenu. “Mutu mwenye nguvu akiwa na silaha anapolinda nyumba yake, mali yake inabaki katika usalama. Lakini mutu mwingine mwenye nguvu zaidi akimushambulia na kumushinda, anamunyanganya silaha zake alizotegemea na kugawanya vitu vya unyanganyi anavyokuwa navyo. “Asiyekuwa wa upande wangu ni adui yangu; na asiyekusanya pamoja nami, anasambaza. “Wakati pepo amekwisha kutoka ndani ya mutu, anazungukazunguka kwenye ukiwa katika jangwa akitafuta nafasi ya kupumzikia. Asipopata nafasi ile, anasema: ‘Nitarudia ndani ya nyumba yangu nilimotoka.’ Anaporudia, anaikuta wazi bila mutu, nayo imefagiliwa na kupambwa vizuri. Halafu anakwenda kutwaa pepo wengine saba wanaokuwa wabaya kumupita, nao wanaingia na kukaa mule. Na hali ya mwisho ya mutu yule inageuka mbaya kuliko hali yake ya kwanza.” Yesu alipokuwa akisema maneno hayo, mwanamuke mumoja kati ya kundi la watu akasema kwa sauti kubwa: “Heri mwanamuke yule aliyekuzaa na kukunyonyesha!” Lakini Yesu akajibu: “Heri zaidi wale wanaosikia neno la Mungu na kulitii!” Wakati watu wengi walipokuwa wakikusanyika pembeni ya Yesu, yeye akaanza kusema: “Watu wa kizazi hiki kibaya wanataka kuona kitambulisho. Lakini hawataonyeshwa kitambulisho isipokuwa kitambulisho cha Yona. Kwa maana kama vile Yona alivyokuwa kitambulisho kwa watu wa Ninawe, ni vile Mwana wa Mutu atakavyokuwa kitambulisho kwa watu wa kizazi hiki. Vilevile kwa Siku ya hukumu, Malkia toka Kusini atasimama na watu wa kizazi hiki na kuwashitaki, kwa sababu yeye alitoka mbali sana kuja kusikiliza maneno ya hekima ya mufalme Solomono. Hapa kuna yule anayekuwa mukubwa kupita Solomono! Kwa Siku ya hukumu, watu wa Ninawe watasimama nanyi watu wa kizazi hiki na kuwashitaki, kwa sababu wao waligeuka toka zambi zao waliposikia mahubiri ya Yona! Hapa kuna yule anayekuwa mukubwa kupita Yona! “Hakuna mutu anayewakisha taa na kuificha au kuifunika na kitunga; lakini anaiweka juu ya kinara kusudi wanaoingia ndani wapate kuona mwangaza. Jicho ni taa ya mwili. Kama jicho lako likiwa zima, mwili wako wote utabaki katika mwangaza. Lakini kama jicho lako linaharibika, mwili wako vilevile utabaki katika giza. Ujiangalie vizuri kusudi mwangaza unaokuwa ndani yako usigeuke kuwa giza. Basi kama mwili wako wote uko katika mwangaza pasipo kiungo kinachokuwa katika giza, mwili wako wote utabaki katika mwangaza kabisa, kama vile taa inavyokuangazia kwa mwangaza wake.” Yesu alipomaliza kusema, Mufarisayo mumoja akamwalika kwake kuja kula chakula. Yesu akaenda na kuikaa kule. Mufarisayo yule akashangaa alipoona kwamba Yesu hakunawa mikono mbele ya kula. Halafu Bwana akamwambia: “Ninyi Wafarisayo ni kama mutu anayesafisha tu inje ya kikombe na sahani; lakini ndani yenu mumejaa tamaa ya wizi na uovu. Ninyi wapumbafu! Si Mungu aliyeumba inje ya mutu ndiye aliyeumba ndani yake vilevile? Basi muwasaidie wamasikini na vitu vya ndani, na vingine vyote vitakuwa safi kwenu. “Ole kwenu, ninyi Wafarisayo! Munatoa fungu moja la kumi la vijani vya kukoleza chakula na kila namna ya mboga; lakini mumezarau haki na upendo wa Mungu. Mambo hayo ndiyo mulipaswa kushika pasipo kuacha mengine. “Ole kwenu, ninyi Wafarisayo! Munapenda kuikaa katika viti vya mbele ndani ya nyumba ya kuabudia na kusalimiwa kwa heshima kwenye nafasi za makutano. Ole kwenu! Munafanana na makaburi yasiyoonekana wazi ambayo watu wanatembea juu yao pasipo kujua.” Mumoja kati ya walimu wa Sheria akamwambia: “Mwalimu, kwa kusema vile unatutukana sisi vilevile.” Yesu akajibu: “Ole kwenu vilevile, ninyi walimu wa Sheria! Munawabebesha watu mizigo mizito, lakini ninyi wenyewe hamufikiri hata kidogo juu ya namna ya kuwasaidia kuibeba. Ole kwenu! Munajenga makaburi ya manabii, wale waliouawa na babu zenu. Kwa hiyo, ninyi munashuhudia na kukubaliana na babu zenu; kwa sababu wao waliwaua wale manabii, na ninyi munawajengea makaburi. Kwa sababu hii, Mungu anasema katika hekima yake: ‘Nitawatumia manabii na mitume; watawaua wamoja kati yao na kuwatesa wengine wao.’ Basi watu wa kizazi hiki watabeba lazima ya damu ya manabii wote iliyomwangwa tangu kuumbwa kwa dunia, tangia kuuawa kwa Abeli mpaka kuuawa kwa Zakaria kwenye hekalu katikati ya mazabahu na Pahali Patakatifu. Kweli ninawaambia: watu wa kizazi hiki watabeba lazima ya mambo hayo yote. “Ole kwenu, ninyi walimu wa Sheria! Mumewaficha watu ufunguo wasiingie kwenye nafasi wanapoweza kujifunza elimu. Ninyi wenyewe hamuingii pale, nanyi munawazuia wale wanaotaka kuingia.” Yesu alipoondoka katika nyumba ya yule Mufarisayo, walimu wa Sheria na Wafarisayo wakaanza kumushambulia vikali sana na kumwuliza maneno mengi wakimupima kusudi wapate kumunasa katika masemi yake. Wakati ule ule makundi mengi ya maelfu ya watu walikusanyika hata wakakanyaganakanyagana. Yesu akaanza kwanza kusema na wanafunzi wake, akiwaambia: “Mufanye angalisho na chachu ya Wafarisayo, maana yake unafiki wao. Hakuna kitu chochote kinachofichwa kitakachokosa kuvumbulikana wala hakuna siri itakayokosa kujulikana. Ni hivi maneno yote mutakayosema katika giza yatasikilika muchana kati. Vilevile maneno yote mutakayosema kwa siri ndani ya chumba chenye kufichama, yatatangazwa juu ya paa la nyumba. “Ninawaambia ninyi warafiki zangu: musiwaogope wale wanaoua mwili tu lakini hawawezi kufanya kitu kingine zaidi. Nitawaonyesha yule munayepaswa kumwogopa; mumwogope Mungu, kwa sababu kisha kuuawa ni yeye anayekuwa na uwezo wa kumutupa mutu katika jehenamu. Hakika ninawaambia, ni huyo munayepaswa kumwogopa! “Ndege watano wadogo, si wanauzishwa kwa bei chini kabisa? Hata vile Mungu hasahau hata mumoja wao. Lakini hata nywele za vichwa vyenu zimehesabiwa zote. Basi musiogope kwa sababu ninyi ni bora zaidi kuliko ndege wengi! “Nami ninawaambia: kila mutu anayenikubali mbele ya watu, Mwana wa Mutu atamukubali vilevile mbele ya wamalaika wa Mungu. Lakini mutu yeyote anayenikana mbele ya watu, yule atakanwa mbele ya wamalaika wa Mungu. “Na kila mutu anayesema vibaya juu ya Mwana wa Mutu atasamehewa, lakini kila mutu anayemutukana Roho Mutakatifu, hatasamehewa. “Wakati watakapowapeleka kwa kuhukumiwa katika nyumba za kuabudia, au mbele ya watawala na ya wakubwa, musijihangaishe juu ya maneno mutakayojibu au yale mutakayosema, kwa sababu Roho Mutakatifu atawafundisha saa ile ile maneno munayopaswa kusema.” Mutu mumoja katika kundi akamwambia Yesu: “Mwalimu, umwambie ndugu yangu anipe sehemu yangu ya urizi, baba aliotuachia.” Yesu akamujibu: “Ewe bwana, ni nani aliyeniweka kuwa mwamuzi wenu au mutu wa kuwagawanyia mali zenu?” Kisha Yesu akawaambia watu wote: “Muangalie, mujilinde na tamaa yote ya mali, kwa sababu mali haiwezi kukinga uzima wa mutu, hata akiwa tajiri sana.” Halafu akawaambia mufano huu: “Kulikuwa tajiri mumoja aliyekuwa na shamba lenye kutoa mavuno mengi. Yeye akawaza na kusema: ‘Nitafanya nini hivi ninakosewa nafasi ya kuwekea mavuno yangu yote?’ Kisha akajisemesha: ‘Nitafanya hivi: nitabomoa gala zangu na nitajenga zingine kubwa zaidi, na mule nitaweka mavuno yangu yote na mali zangu zingine.’ Kisha nitajisemesha hivi juu yangu mwenyewe: ‘Uko na mali nyingi ulizoweka akiba kwa miaka mingi. Sasa utulizane, ukule na kunywa na kujifurahisha.’ Lakini Mungu akamwambia: ‘Mupumbafu wewe! Leo leo usiku utakufa. Na sasa, vitu hivi vyote ulivyojitayarishia vitakuwa vya nani?’ ” Yesu akaongeza kusema: “Ni hivi inavyokuwa kwa yule anayejiwekea mali mengi, lakini mbele ya Mungu hahesabiwi kuwa na kitu.” Kisha Yesu akawaambia wanafunzi wake: “Ni kwa sababu hii ninawaambia: musijisumbue kwa ajili ya maisha yenu, kwamba mutakula nini; wala musijisumbue kwa ajili ya miili yenu, kwamba mutavaa nini. Uzima unapita chakula, nao mwili ni wa lazima kuliko nguo. Mufikiri juu ya kibombobombo: ndege hao hawapandi mbegu, hawavuni, hawana gala wala nafasi yoyote ya kuwekea mavuno, lakini Mungu anawalisha. Ninyi ni wa lazima zaidi kuliko ndege! Nani kati yenu, kwa ajili ya kujisumbua kwake, anaweza kujiongezea hata siku moja kupita muda wa maisha yake? Basi ikiwa hamuwezi kufanya kitu kidogo kama hiki, kwa nini munajisumbua juu ya vitu vingine? Mufikiri juu ya namna maua yanavyoota. Hayasumbuki wala kujisukia nguo. Lakini ninawaambia kwamba hata mufalme Solomono katika utukufu wote aliokuwa nao, hakuvaa nguo inayoweza kulinganishwa na uzuri wa moja la maua. Basi ikiwa Mungu anavalisha majani kama hivi, yanayoonekana pale leo na kesho yanatoweka na kutupwa, hatawavalisha vizuri zaidi ninyi wenye imani ndogo? Basi musijisumbue kwa kutafuta chakula au kinywaji. Ni wapagani ndio wanaotafutatafuta vitu hivyo vyote. Baba yenu anajua kwamba munahitaji vitu hivyo. Hivi ninyi mutafute Ufalme wake, naye atawaongezea vitu hivi vyote. “Musiogope ninyi kundi dogo! Kwa kuwa Baba yenu amependelea kuwapa ninyi ule Ufalme wake. Muuzishe vitu munavyokuwa navyo, muwasaidie wamasikini. Mujiwekee feza zisizoweza kuwa na upungufu, nayo akiba isiyoweza kumalizika katika mbingu. Kule wizi hawawezi kukaribia wala nondo hawaharibu. Kwa maana pahali akiba yenu inapokuwa, ni pale roho zenu zinapokuwa vilevile. “Mukuwe tayari kwa kutumika na kuacha taa zenu zikiwaka. Mukuwe kama watumishi wanaomungojea bwana wao arudie kutoka katika karamu ya ndoa, kusudi wakati anapofika na kupiga hodi wamufungulie mulango mara moja. Heri watumishi wale bwana wao atakaowakuta wakikesha wakati anapofika! Kweli ninawaambia: atafunga mukaba wake vizuri na kuwakaribisha kula chakula, na kubakia pale akiwashugulikia. Heri watumishi wale atakaowakuta wakikesha hata akifika katikati ya usiku au nyuma ya saa ile. Munajua vema kwamba mwenye nyumba angejua saa gani mwizi atakapokuja kumwiba, asingeacha nyumba yake ibomolewe. Kwa hiyo ninyi vilevile mukuwe tayari, kwa sababu Mwana wa Mutu atarudia saa musiyozania.” Halafu Petro akamwuliza Yesu: “Bwana, mufano huu unatuelekea sisi wenyewe au unawaelekea watu wote?” Bwana akajibu: “Ni nani basi anayekuwa musimamizi mwaminifu na mwenye akili? Ni yule bwana wake aliyemuweka kwa kuwasimamia watumishi wake wengine na kumwamuru kuwapatia posho lao kwa wakati uliopangwa. Heri mutumishi yule, ikiwa saa bwana wake anaporudia, anamukuta akifanya kazi ile. Kweli ninawaambia: bwana wake atamuweka mutumishi yule kuwa musimamizi wa mali yake yote. Lakini kama mutumishi yule akijisemesha mwenyewe kwamba bwana wake anakawia kurudia; na halafu anaanza kuwapiga watumishi wenzake, wanaume na wanawake, naye anakula na kunywa na kulewa. Basi bwana wa mutumishi yule atakuja siku asiyozania, na saa asiyoijua. Naye atamupiga vikali na kumwazibu sawa na watu wasiokuwa waaminifu. “Mutumishi anayejua mapenzi ya bwana wake, lakini anakosa kujiweka tayari na kutofanya sawa na mapenzi ya bwana yule, atapigwa fimbo nyingi. Lakini kwa ngambo ingine, yule asiyejua mapenzi ya bwana yake, na anayefanya mambo yanayostahili azabu, atapigwa fimbo chache. Kwa maana kila mutu aliyepewa vingi, ataombwa kutoa vingi zaidi; na aliyepewa madaraka mengi, ataulizwa mengi zaidi. “Nimekuja kuleta moto katika dunia, nami ningetaka sana kuona ukiwa umekwisha kuwaka! Niko na muzigo wa mateso ninaopaswa kubeba, nami ninasongwa sana mpaka mapaswa hayo yatakapotimizwa! Munazania kwamba mimi nimekuja kuleta amani katika dunia? Ninawaambia ninyi: si vile, nimekuja kuleta matengano. Kwa maana tangu sasa watu watano wa jamaa moja watatengana; watatu watapingana na wawili, na wawili watapingana na watatu. Baba atapingana na mwana wake, na mwana atapingana na baba yake. Mama atapingana na binti yake, na binti atapingana na mama yake. Mama mukwe atapingana na muke wa mutoto wake, na muke yule atapingana na mama mukwe yake.” Yesu akawaambia makundi vilevile: “Wakati munapoona mawingu yakitokea upande wa magaribi, mara moja munasema kwamba mvua itanyesha, na ni vile inavyokuwa. Na wakati munapoona upepo ukivuma toka upande wa kusini, munasema kwamba jua litakuwa kali, na ni vile inavyokuwa. Ninyi wanafiki! Munajua kutambua hali ya inchi na ya anga, namna gani munashindwa kutambua nyakati hizi za sasa? “Sababu gani ninyi wenyewe hamuwezi kujiamulia jambo la haki? Unapokwenda kwa tribinali na mupinzani wako, ujikaze upatane naye mungali katika njia. Kama si vile atakupeleka mbele ya mwamuzi, na mwamuzi atakutoa kwa askari, na askari atakutupa katika kifungo. Ninakuambia: hautatoka mule mpaka utakapomaliza kulipa sengi la mwisho.” Katika siku zile watu wamoja wakakuja kumwelezea Yesu habari juu ya wale watu wa Galilaya waliouawa na liwali Pilato walipokuwa wakichinja nyama za kutolea Mungu sadaka. Yesu akawauliza: “Munazani kwamba Wagalilaya hawa waliuawa vile kwa sababu wao walikuwa wenye zambi kuliko Wagalilaya wengine wote? Hakika si vile, lakini musipogeuka toka zambi zenu, ninyi wote mutaangamia kama wao. Vilevile munazani kwamba wale watu kumi na wanane waliokufa munara ulipowaangukia kule Siloamu, walikuwa wakosaji kuliko wakaaji wengine wote wa Yerusalema? Hakika si vile: lakini musipogeuka toka zambi zenu, ninyi wote mutaangamia kama wao.” Kisha Yesu akawaambia mufano huu: “Mutu mumoja alikuwa na muti wa tini uliopandwa katika shamba lake la mizabibu. Alikuja kutafuta matunda juu yake, lakini hakupata kitu. Basi akamwambia mutunzaji wa hili shamba: ‘Sasa ni muda wa miaka mitatu ninakuja kutafuta matunda juu ya muti huu wa tini nami sipati kitu. Uukate! Muti huu unaharibu udongo bure.’ Lakini yule mutunzaji wa shamba akajibu: ‘Bwana, uuache tena mwaka huu; nitalima pembenipembeni yake na kuutilia mboleo. Hivi utaweza labda kutoa matunda mwaka kesho! Kama si vile, basi utaukata!’ ” Siku moja ya Sabato, Yesu alikuwa akifundisha katika nyumba ya kuabudia. Na mule ndani mulikuwa mwanamuke mumoja mugonjwa, aliyeshikwa na pepo kwa muda wa miaka kumi na minane. Mugongo wake ulikuwa umekunjama na hakuweza kuinuka hata kidogo. Yesu alipomwona yule mwanamuke, akamwita, akamwambia: “Ewe mama, ugonjwa wako umepona.” Halafu akaweka mikono juu yake kwa kumuponyesha. Na mara moja akainuka tena, na kumutukuza Mungu. Lakini mukubwa wa nyumba ya kuabudia alichukizwa kwa sababu Yesu aliponyesha mutu kwa siku ya Sabato. Kwa hiyo akawaambia watu waliokusanyika pale: “Kuna siku sita za kazi. Basi mufike kwa kuponyeshwa katika siku zile, hapana kwa siku ya Sabato!” Lakini Bwana akamujibu: “Ninyi wanafiki! Kuna mutu mumoja kati yenu anayekosa kumufungua ngombe au punda wake toka katika upango kwa siku ya Sabato kwa kumupeleka kunywa maji? Sasa, mwanamuke huyu anayekuwa wa uzao wa Abrahamu, ambaye alifungwa na Shetani kwa muda wa miaka kumi na minane, haikumupasa afunguliwe katika kifungo hiki ingawa ni siku ya Sabato?” Yesu aliposema vile, wapinzani wake wote wakafezeheka, lakini kundi lote la watu wote walifurahia matendo yote ya ajabu aliyoyatenda. Yesu akasema tena: “Ufalme wa Mungu unafanana na nini? Nitaulinganisha na nini? Unafanana na mbegu ya haradali mutu mumoja aliyotwaa na kuipanda katika shamba lake. Ikaota na kuwa muti mukubwa, nao ndege wakakuja kujenga chicha zao katikati ya matawi yake.” Yesu akasema tena: “Nitafananisha Ufalme wa Mungu na nini? Unafanana na chachu mwanamuke mumoja aliyoitwaa na kuichanga na vipimo vitatu vya unga kwa kuponda mikate, hata yote ikapata kuvimba.” Yesu alipokuwa katika safari kwenda Yerusalema, alipita katika miji na vijiji akifundisha. Mutu mumoja akamwuliza: “Bwana, ni watu wachache tu ndio watakaookolewa?” Halafu Yesu akawaambia: “Mufanye nguvu muingie kwa kupitia mulango unaokuwa mwembamba; maana ninawaambia ninyi hakika: watu wengi watajaribu kuingia lakini hawataweza. “Mwenye nyumba atakapokwisha kusimama na kufunga mulango, ninyi mutabaki inje na kuanza kupiga hodi na kusema: ‘Bwana, utufungulie.’ Naye atawajibu: ‘Sijui munatokea wapi.’ Halafu mutaanza kumwambia: ‘Sisi tulikula na kunywa pamoja nawe, na wewe ulifundisha katika barabara za muji wetu.’ Lakini atawaambia tena: ‘Sijui munatokea wapi. Mutoke karibu nami, ninyi wote watenda maovu!’ Na kule mutalia na kusaga meno, mutakapowaona Abrahamu, Isaka, Yakobo na manabii wote katika Ufalme wa Mungu. Lakini ninyi mutakuwa mumetupwa inje! Watu watakuja toka mashariki na magaribi, kaskazini na kusini, nao wataikaa kula chakula katika Ufalme wa Mungu. Wanaokuwa wa mwisho, watakuwa wa kwanza na wa kwanza watakuwa wa mwisho.” Kwa saa zile Wafarisayo wamoja walimwendea Yesu na kumwambia: “Ondoka hapa uende fasi ingine, maana mufalme Herode anataka kukuua.” Yesu akawajibu: “Mwende kumwambia yule mbweha: ‘Leo na kesho nitafukuza pepo na kuponyesha wagonjwa, na kesho kutwa nitamaliza kazi yangu.’ Lakini ninapaswa kuendelea na safari yangu leo, kesho na kesho kutwa, kwa sababu haipaswi nabii auawe inje ya Yerusalema. “Ewe Yerusalema, Ewe Yerusalema, wewe unayewaua manabii na wajumbe ambao Mungu anakutumia kwa kuwatupia mawe. Mara nyingi nilitaka kuwakusanya wakaaji wako kama vile kuku anavyokusanya vitoto vyake chini ya mabawa yake, lakini ninyi hamukutaka! Makao yenu yataachwa ukiwa. Lakini ninawaambia: tangia sasa hamutaniona tena mpaka mutakaposema: ‘Abarikiwe huyu anayekuja kwa jina la Bwana.’ ” Siku moja ya Sabato, Yesu aliingia katika nyumba ya mumoja wa wakubwa wa Wafarisayo kwa kula chakula. Mule watu wakabaki wakimuchunguza. Na mbele ya Yesu kulikuwa mutu mumoja aliyekuwa na ugonjwa wa kuvimba tumbo. Basi Yesu akawauliza walimu wa Sheria na Wafarisayo: “Sheria inaruhusu au inakataza kuponyesha mutu kwa siku ya Sabato?” Lakini wao wakanyamaza. Halafu Yesu akamushika mugonjwa, akamuponyesha na kumuruhusu kwenda. Kisha akawaambia wale watu: “Ni nani kati yenu mutoto wake au ngombe wake akitumbukia ndani ya kisima, atakayekosa mara moja kumwondosha mule hata ikiwa ni siku ya Sabato?” Nao hawakuweza kumujibu neno. Yesu alipoona namna wale walioalikwa walivyojichagulia viti vya heshima, akawaambia mufano huu: “Wakati mutu anapokualika kwa karamu ya ndoa, usiikae kwenye viti vya mbele. Labda kati ya waalikwa kuna mutu mwenye heshima kukupita. Naye anapokuja, yule aliyewaalika ninyi wawili, ataweza kuja kukuambia: ‘Umwachie mutu huyu kiti.’ Halafu utapatwa na haya kwenda kuikaa kwenye viti vya nyuma. Lakini wakati unapoalikwa, kwenda kuikaa kwenye viti vya nyuma, kusudi wakati yule aliyekualika atakapokuja, akuambie: ‘Rafiki, jongea huku mbele zaidi.’ Na halafu utaheshimiwa mbele ya wote unaoikaa pamoja nao kwa kula. Kwa maana kila mutu anayejiinua atashushwa, lakini anayejishusha atainuliwa.” Kisha Yesu akamwambia yule aliyemwalika: “Wakati unapofanya karamu ya muchana au ya magaribi, usiwaalike warafiki zako, wala wandugu zako, wala watu wa jamaa yako, wala jirani zako wanaokuwa watajiri, kusudi nao vilevile wasikualike, nawe usikuwe kama umelipwa. Lakini wakati unapofanya karamu, uwaalike wamasikini, vilema, viwete na vipofu. Hivi utabarikiwa, kwa maana watu hawa hawana cha kukulipa. Utalipwa hayo yote wakati wenye haki watakapofufuka.” Mutu mumoja kati ya wale waliokuwa wakiikaa kula pamoja na Yesu aliposikia maneno hayo, akamwambia: “Heri mutu atakayeshiriki kwa kula karamu katika Ufalme wa Mungu!” Halafu Yesu akawaambia mufano huu: “Mutu mumoja alifanya karamu kubwa, na kualika watu wengi. Saa ya karamu ilipotimia akamutuma mutumishi wake kwenda kuwaambia walioalikwa kwamba wafike kwa maana vitu vyote viko tayari. Lakini wao wote moja kwa moja wakaanza kutoa sababu zao za kutokufika. Wa kwanza akamwambia yule mutumishi: ‘Nimenunua shamba, nami ninapaswa kwenda kuliangalia. Tafazali, unisamehe.’ Mwingine akamwambia: ‘Nimenunua ngombe kwa ajili ya kazi ya kulima, nami ninakwenda kuwapima. Tafazali, unisamehe.’ Na mwingine akamwambia: ‘Mimi ninatoka kuoa siku hizi, na kwa sababu hii siwezi kuja.’ Basi yule mutumishi akarudia na kumwelezea bwana wake maneno hayo yote. Halafu bwana wa nyumba akakasirika, na kumwambia: ‘Kwenda upesi katika nafasi za mukutano na katika barabara za muji, uwalete wamasikini, vilema, vipofu na viwete na kuwaingiza humu.’ Kisha, yule mutumishi akarudia na kusema: ‘Bwana, nimetimiza sawa ulivyoniamuru, lakini kungali nafasi.’ Halafu bwana wake akamwambia: ‘Kwenda katika njia kwenye vijiji na pembeni ya mashamba, uwalazimishe watu wafike kuingia, kusudi nyumba yangu ipate kujaa. Kwa maana ninawaambia kwamba kati ya wale niliokuwa nimewaalika, hakuna hata mumoja wao atakayeonja vyakula vya karamu yangu.’ ” Siku moja makundi mengi ya watu walikuwa wakimufuata Yesu nyuma. Yeye akageuka na kuwaambia: “Mutu anayenifuata, atakuwa kweli mwanafunzi wangu kama akinipendelea mimi kuliko baba na mama yake, muke na watoto wake, wakaka na wadada zake. Na zaidi ya hii hapaswi kujipendelea yeye mwenyewe vilevile. Mutu yeyote asiyejitolea kwa kubeba musalaba wake na kunifuata, hawezi kuwa mwanafunzi wangu. Ni nani kati yenu anayetaka kujenga munara, atakayekosa kwanza kuikaa na kuhesabu mali yote atakayoitumia kwa kujenga kusudi ajue kama yuko na mali inayotosha kwa kumaliza? Kwa maana akiweka musingi, na nyuma anashindwa kumaliza kujenga munara ule, wote wanaoona jambo lile wataanza kumuzarau, wakisema: ‘Mutu huyu alianza kujenga, lakini hakuweza kumaliza!’ Au ni mufalme gani anayetaka kwenda kupigana vita na mufalme mwingine, atakayekosa kwanza kuikaa na kujiuliza kama kwa nguvu za waaskari wake elfu kumi ataweza kumushinda adui yake anayekuja na waaskari elfu makumi mbili? Yeye akiona kwamba hataweza, atamutumia yule mufalme mwingine ujumbe kwa kuomba mapatano ya amani, huyo mwingine anapokuwa angali mbali. Ni vile inavyokuwa, hakuna mumoja wenu atakayeweza kuwa mwanafunzi wangu kama asipoacha vyote anavyokuwa navyo.” “Chumvi ni kitu kizuri. Lakini chumvi ikipoteza onjo lake, itatiwa nini kusudi ipate tena kukolea? Haifai tena kitu wala kwa udongo wala kwa mboleo, lakini watu wanaitupa tu. Mwenye kuwa na masikio ya kusikia, asikie!” Siku moja walipishaji wa kodi na watenda mabaya wengi walikusanyika karibu na Yesu kwa kumusikiliza. Wafarisayo na walimu wa Sheria wakaanza kunungunika, wakisema: “Mutu huyu anawakaribisha watenda mabaya na kula pamoja nao!” Halafu Yesu akawaambia mufano huu: “Ni nani kati yenu akiwa na kondoo mia moja, na mumoja wao akipotea, atakayekosa kuwaacha wale wengine makumi tisa na tisa kwenye mashamba ya kulishia wanyama na kwenda kumutafuta yule aliyepotea mpaka atakapomupata? Atakapomwona, atamubeba kwa furaha juu ya mabega. Naye anaporudia kwake, atawaita warafiki na jirani zake na kuwaambia: ‘Mufurahi pamoja nami, kwa sababu nimemupata kondoo wangu aliyepotea!’ Vilevile ninawaambia, ndivyo kutakuwa furaha kubwa zaidi mbinguni kwa ajili ya mwenye zambi mumoja anayegeuka toka zambi zake, kuliko wenye haki makumi tisa na tisa wasiokuwa na lazima ya kugeuka toka zambi zao. “Vilevile ni mwanamuke gani anayekuwa na vikoroti kumi vya feza, naye akipoteza kimoja, atakayekosa kuwakisha taa na kufagia nyumba kutafuta vizuri mpaka akipate? Anapokipata atawaita warafiki na jirani zake na kuwaambia: ‘Mufurahi pamoja nami kwa sababu nimepata kikoroti kile cha feza nilichokipoteza!’ Vilevile ninawaambia, ndivyo wamalaika wa Mungu wanavyofurahi kwa ajili ya mwenye zambi mumoja anayegeuka toka zambi zake.” Yesu akaendelea kuwaambia mufano mwingine: “Mutu mumoja alikuwa na wana wawili. Yule mudogo akamwambia baba yake: ‘Baba, unipe ile sehemu ya urizi inayopaswa kuwa yangu.’ Basi baba akagawanya mali yake kati ya wana wake wote wawili. Nyuma ya siku chache, yule mudogo akauzisha urizi wake na kwenda katika inchi ya mbali. Kule aliponda mali yake yote katika maisha ya ovyo. Alipokwisha kumaliza mali yake yote, njaa kubwa ikatokea katika inchi ile, akaanza kuishi katika ukosefu. Kwa hiyo akaenda kuomba kazi kwa mukaaji mumoja wa inchi ile. Mukaaji yule akamutuma katika mashamba yake kufanya kazi ya kukulisha nguruwe. Naye alitamani sana kula maganda yale nguruwe waliyokula, lakini hakuna mutu aliyemupa nayo. Basi akaanza kufikiri yeye mwenyewe na kujisemesha: ‘Watumishi wote wa baba yangu wana vyakula kwa uwingi, nami huku ninakufa na njaa! Basi nitaondoka huku na kurudia kwa baba yangu nami nitamwambia: baba, nimemukosea Mungu na nimekukosea wewe vilevile. Sababu hii sistahili kuhesabiwa tena sawa vile mwana wako; unihesabu sawa vile mumoja wa watumishi wako.’ Kisha akafunga safari yake na kurudia kwa baba yake. “Alipokuwa angali mbali kidogo, baba yake akamwona, akamusikilia huruma. Akamukimbilia, akamukumbatia mwana wake na kumubusu. Mwana wake akamwambia: ‘Baba, nimemukosea Mungu na nimekukosea wewe vilevile. Sababu hii sistahili kuhesabiwa tena sawa vile mwana wako.’ Lakini baba yake akawaambia watumishi wake: ‘Mulete mbio kanzu nzuri sana na kumuvalisha nayo. Mumuvalishe pete kwenye kidole chake na mumuvalishe viatu. Kisha, mulete yule ngombe mwenye kunona na kumuchinja; nasi tutakula na kufurahi pamoja. Kwa sababu mwana wangu huyu alikuwa amekufa, na amefufuka, alikuwa amepotea na sasa ameonekana.’ Nao wakaanza kufurahi pamoja. “Kwa wakati ule, mwana wake wa kwanza alikuwa kwenye mashamba. Alipokuwa akirudia na kukaribia nyumba, akasikia sauti ya watu wakiimba na kucheza. Akamwita mumoja kati ya watumishi, na kumwuliza juu ya mambo yanayopitika kule. Mutumishi ule akamujibu: ‘Mudogo wako amerudia salama; kwa hiyo baba yako amechinja yule ngombe mwenye kunona.’ Ndugu huyu mukubwa akakasirika na kukataa kuingia ndani ya nyumba. Basi baba yake akatoka inje na kumusihi aingie. Lakini akamujibu baba yake: ‘Ninakutumikia kwa miaka mingi na sijakukosea hata mara moja. Ingawa vile haujanipatia hata kitoto cha mbuzi kusudi nifurahi pamoja na warafiki zangu. Lakini mwana wako huyu aliyeharibu mali yako katika ukahaba alipofika, ukamuchinjia yule ngombe mwenye kunona!’ Baba yake akamwambia: ‘Mutoto wangu, wewe uko pamoja nami siku zote na kile ninachokuwa nacho ni chako. Kwa hivi ilitupasa kushangilia na kufurahi, kwa maana mudogo wako huyu alikuwa amekufa na amefufuka, alikuwa amepotea na sasa ameonekana.’ ” Yesu akawaambia wanafunzi wake mufano huu: “Kulikuwa mutu mumoja tajiri aliyekuwa na mulinzi wa mali yake. Yule mulinzi akachongewa kwa bwana wake kwamba anaponda mali yake. Halafu bwana wake akamwita na kumwambia: ‘Ni habari gani ile waliyonielezea juu yako? Ninakuomba unifanyie hesabu yote ya mali yangu, kwa sababu hauwezi tena kuwa mulinzi wa mali yangu.’ Yule mulinzi akajiuliza: ‘Sasa nitafanya nini? Bwana wangu ananifukuza kwa kazi. Kulima, mimi siwezi; na kuombaomba, ninasikia haya. Sasa ninajua jinsi nitakavyofanya kusudi wakati nitafukuzwa kwa kazi yangu ya ulinzi, watu wapate kunikaribisha katika nyumba zao.’ Halafu akamwita kila mutu aliyekuwa na deni ya bwana wake. Akamwuliza kwanza: ‘Deni ya bwana wangu unayokuwa nayo ni yapata gani?’ Naye akamujibu: ‘Madebe mia moja ya mafuta ya muzeituni.’ Yule mulinzi wa mali akamwambia: ‘Kamata barua yako ya mapatano ya deni, ikaa upesi na uandike makumi tano.’ Kisha akamwuliza mwingine: ‘Na wewe uko na deni yapata gani?’ Naye akajibu: ‘Saki mia moja za ngano.’ Yule mulinzi akamwambia: ‘Kamata barua yako ya mapatano na uandike saki makumi nane.’ Basi bwana wa yule mulinzi akamusifu kwa sababu alitenda kwa werevu. Kwa maana watu wa dunia hii wanatengeneza maneno yao na wenzao kwa werevu sana kuliko watu wanaopenda kuishi katika mwangaza.” Yesu akaongeza kusema: “Nami ninawaambia: mutumie mali ya dunia hii kwa kuunga urafiki, kusudi wakati mali ile itakapokosekana, mupate kupokelewa kwenye makao ya milele. Yule anayekuwa mwaminifu katika vitu vichache, yuko mwaminifu vilevile katika vitu vingi. Na yule asiyekuwa mwaminifu katika vitu vichache, hayuko mwaminifu vilevile katika vitu vingi. Basi kama ninyi hamukukuwa waaminifu kwa kulinda mali ya dunia hii, ni nani atakayeweza kuwatumainia kwa kulinda mali ya kweli? Na kama hamuwezi kulinda mali ya mutu mwingine kwa uaminifu, ni nani atakayewapa mali yenu ya pekee? “Hakuna mutumishi anayeweza kutumikia wabwana wawili. Kwa maana atamuchukia mumoja na kumupenda mwingine; au atashikamana na mumoja na kumuzarau mwingine. Hamuwezi kumutumikia Mungu na kutumikia mali vilevile.” Wakati Wafarisayo waliposikia maneno haya yote wakamuzarau Yesu, kwa sababu walikuwa wapenda feza. Yesu akawaambia: “Ninyi ni watu wanaojionyesha kuwa wenye haki mbele ya watu, lakini Mungu anajua yanayokuwa ndani ya mioyo yenu. Kwa maana mambo yanayosifiwa na watu ni machukizo mbele ya Mungu. “Sheria ya Musa na maandiko ya manabii yalitangazwa mpaka kuja kwa Yoane. Tangu wakati ule, Habari Njema ya Ufalme wa Mungu inahubiriwa, na kila mutu anajiingiza kwa kinguvu ndani ya ufalme ule. Lakini ni vyepesi zaidi kwa mbingu na dunia kutoweka kuliko hata nukta moja ya Sheria kuondoshwa. “Kila mutu anayemufukuza muke wake na kuoa mwingine, anazini; na mutu anayemwoa yule muke aliyefukuzwa anazini vilevile. “Kulikuwa mutu mumoja tajiri aliyezoea kuvaa nguo zenye kuwa laini sana za bei kali zaidi na aliyeishi katika raha siku zote. Vilevile kulikuwa masikini mumoja aliyeitwa Lazaro aliyekuwa na vidonda mwili wote, alibaki akilala mbele ya mulango wa nyumba ya yule tajiri. Yeye alikuwa akitamani kula makombo yaliyoanguka toka juu ya meza ya yule tajiri. Hata imbwa walikuja kulambulalambula vile vidonda vyake. Siku moja yule masikini akakufa, na wamalaika wakamupeleka mpaka pembeni ya Abrahamu. Na yule tajiri akakufa vilevile na kuzikwa. Alipokuwa katika jehenamu akiteswa sana, akainua macho, akamwona Abrahamu kwa mbali na Lazaro akiwa pembeni yake. Basi akalalamika, akisema: ‘Baba Abrahamu, unisikilie huruma; umutume Lazaro achovye incha ya kidole chake katika maji, anipoleshe ulimi wangu, kwa sababu ninateswa sana katika moto huu.’ Lakini Abrahamu akamujibu: ‘Mutoto wangu, kumbuka kwamba umekwisha kupewa mema yaliyokupasa wakati ulipoishi katika dunia, na Lazaro alipata taabu. Na sasa yeye anatulizwa, lakini wewe unateswa. Na zaidi ya hii kuna shimo kubwa sana kati yetu na ninyi. Hivi wale wanaokuwa huku wakitaka kufika kule kwenu hawawezi, wala wale wanaokuwa kule hawawezi kuvuka kwa kufika huku kwetu.’ Halafu tajiri akasema: ‘Basi, baba ninakuomba umutume Lazaro kwa nyumba ya baba yangu, kwa maana niko na wandugu watano. Aende kuwaonya, kusudi nao vilevile wasikuje katika nafasi hii ya mateso.’ Abrahamu akajibu: ‘Wandugu zako wako na maandiko ya Musa na ya manabii, wayasikilize!’ Naye tajiri akasema tena: ‘Ee Abrahamu, ile haitoshi. Lakini kama mutu mumoja akifufuka na kuwaendea, watageuka toka katika zambi zao.’ Lakini Abrahamu akamwambia: ‘Kama wandugu zako hawasikilizi maonyo ya Musa na ya manabii, hawatasadiki hata mutu aliyefufuka.’ ” Yesu akawaambia wanafunzi wake: “Sherti mambo ya kuwaangusha watu yatokee, lakini ole kwa mutu yule anayeyaleta! Ingekuwa heri afungiwe jiwe kubwa la kusagia katika shingo na kutumbukizwa ndani ya bahari, kuliko kumwangusha mumoja wa wadogo hawa. Kwa sababu hii mujiangalie vizuri. “Kama ndugu yako akikosa, umwonye, na akigeuka toka katika zambi zake, umusamehe. Kama akikukosea mara saba kwa siku, na akirudia kwako kila mara kwa kukuomba huruma, umusamehe.” Mitume wakamwambia Bwana: “Utuongezee imani.” Bwana akajibu: “Kama mukiwa na imani, hata ikiwa tu kama punje ndogo sana ya haradali, mutaweza kuuambia muti huu wa mukuyu: ‘Ujiongoe hapa na uende kujipanda katika bahari,’ nao ungewatii. “Tuseme kwa mufano, kati yenu kuna mutu mumoja anayekuwa na mutumishi anayemulimia au kumuchungia nyama wake. Mutumishi yule anaporudia toka kwenye shamba ataweza kumwambia kwamba aikae mara moja kula chakula? Si vile, yeye atamwambia kwanza amupigie chakula na kujitayarisha vizuri kusudi amushugulikie mpaka atakapomaliza kula na kunywa. Kisha pale, ataweza kula na kunywa. Basi bwana wa yule mutumishi atamushukuru kwa sababu amefanya sawa vile alivyoamuriwa? Hapana. Na ni hivi inavyokuwa kwenu vilevile. Wakati mutakapokwisha kufanya yote muliyoamuriwa, museme: ‘Sisi ni watumishi tu, tumetimiza tu mapaswa yetu.’ ” Yesu alipokuwa katika safari kwenda Yerusalema, akapita katika jimbo la Samaria na la Galilaya. Alipokuwa akiingia katika kijiji kimoja, watu kumi wenye ukoma wakafika kukutana naye. Walisimama kwa mbali wakilalamika, wakisema: “Yesu Bwana utusikilie huruma!” Yesu alipowaona, akawaambia: “Mwende kwa makuhani kusudi wapate kuwachunguza.” Nao walipokuwa katika njia kwenda kule, wakaponyeshwa. Na mumoja wao alipoona kwamba amekwisha kupona, akarudia akimusifu Mungu kwa sauti kubwa. Akainama uso mpaka chini mbele ya Yesu na kumushukuru. Mutu huyo alikuwa Musamaria. Halafu Yesu akauliza: “Watu walioponyeshwa hawakukuwa kumi? Wale wengine tisa wako wapi? Hakuna mwingine kati yao aliyerudia kwa kumutolea Mungu shukrani, isipokuwa huyu mugeni tu?” Kisha Yesu akamwambia mutu yule: “Simama, ujiendee. Imani yako imekuponyesha.” Wafarisayo wakamwuliza Yesu: “Ufalme wa Mungu utakuja wakati gani?” Akawajibu: “Ufalme wa Mungu unakuja bila kutambulikana wazi. Hawatasema: ‘Anatawala hapa’ au ‘Anatawala huku.’ Hakika Mungu anatawala kati yenu.” Kisha akawaambia wanafunzi wake: “Kutakuwa siku mutakazotamani kumwona tena Mwana wa Mutu kwa muda tu, lakini hamutapata muda ule. Watu watawaambia: ‘Yuko kule!’ au ‘Yuko hapa!’ Lakini musiondoke kwa kuwafuata kule. Kwa maana kama vile umeme unavyoangaza na kuonekana wazi katika mbingu yote, ni vile Mwana wa Mutu atakavyoonekana siku atakapokuja. Lakini kwanza sherti ateswe sana na kukataliwa na watu wa kizazi hiki. Na kama ilivyokuwa katika siku za Noa, ni vile itakavyokuwa katika nyakati za kuja kwa Mwana wa Mutu. Siku zile watu walikuwa wakikula na kunywa, wakioa na kuolewa mpaka ilipotimia siku ile Noa alipoingia ndani ya chombo. Halafu mvua kubwa ikanyesha na kuwaangamiza wote. Ni vile ilivyokuwa katika siku za Loti. Watu walikuwa wakikula na kunywa, wakinunua na kuuzisha, wakipanda mbegu na kujenga. Lakini siku ile Loti alipoondoka Sodoma, moto na kiberiti vikashuka kama mvua toka mbinguni na kuwaangamiza wote. Ni hivi itakavyokuwa siku ile Mwana wa Mutu atakayotokea. “Siku ile, yule atakayekutiwa juu ya paa la nyumba, asishuke ndani yake kwa kukamata vitu vyake. Vilevile yule atakayekutiwa katika shamba, asirudie kwake. Mukumbuke yale yaliyomutokea muke wa Loti. Yule atakayelinda uzima wake, ataupoteza; lakini yule atakayetoa uzima wake, ataulinda. Ninawaambia ninyi: katika usiku ule, watu wawili watakuwa katika kitanda kimoja; mumoja atatwaliwa na mwingine ataachwa. Wanawake wawili watakuwa wakisaga pamoja, mumoja atapelekwa na mwingine ataachwa. [ Watu wawili watakuwa katika shamba moja, mumoja atapelekwa na mwingine ataachwa.]” Wanafunzi wakamwuliza: “Bwana, mambo haya yatafanyika wapi?” Naye akawajibu: “Nafasi patakapokuwa muzoga ni pale tai watakapokusanyika.” Halafu Yesu akawaambia wanafunzi wake mufano huu kwa kuwaonyesha kwamba wanapaswa kuomba siku zote pasipo kuchoka. Akasema: “Katika muji mumoja, kulikuwa mwamuzi mumoja asiyemwogopa Mungu wala kumujali na mutu yeyote. Vilevile katika muji ule, kulikuwa mujane mumoja aliyekuwa akimwendea yule mwamuzi akimusihi: ‘Unipatie haki yangu juu ya mupinzani wangu.’ Kwa muda murefu yule mwamuzi alikataa. Lakini kisha akajiuliza mwenyewe: ‘Ijapokuwa mimi simwogopi Mungu wala simujali mutu yeyote, lakini kwa sababu mujane huyu anazidi kuniuzi nitamupatia haki yake, kusudi asiendelee kufika hapa na kunikasirikisha.’ ” Halafu Bwana akasema: “Musikilize jinsi mwamuzi huyu mubaya anavyosema! Basi, Mungu hatawapatia haki wale wachaguliwa wake wanaomulilia usiku na muchana? Au atakawia kuwasaidia? Ninawaambia ninyi: hatakawia kuwapatia haki. Lakini Mwana wa Mutu atakaporudia, atakuta watu wenye kumwamini katika dunia?” Vilevile Yesu akawaambia mufano huu kwa ajili ya watu waliojiona kuwa wenye haki na kuwazarau wengine. “Siku moja watu wawili walienda kuomba kwenye hekalu; mumoja alikuwa Mufarisayo na mwingine alikuwa mulipishaji wa kodi. Yule Mufarisayo akajitenga na mwenzake akiomba hivi: ‘Ee Mungu, ninakushukuru kwa sababu mimi si kama watu wote wengine wanaokuwa wanyanganyi, watenda maovu, wazinzi. Ninakushukuru vilevile kwa kuwa mimi si kama huyu mulipishaji wa kodi. Ninafunga kula chakula mara mbili kila juma na ninatoa fungu moja la kumi la vitu vyote ninavyopata.’ Lakini yule mulipishaji wa kodi alisimama kwa mbali, naye hakusubutu hata kuinua macho yake kuelekea mbingu; lakini alijipigapiga kwa huzuni na kusema: ‘Ee Mungu, unisamehe mimi mutenda mabaya.’ ” Yesu akaongeza kusema: “Ninawaambia kwamba mutu huyu alirudia kwake akiwa amehesabiwa kuwa na haki mbele ya Mungu, lakini si yule Mufarisayo. Kwa maana kila mutu anayejiinua atashushwa, lakini anayejishusha atainuliwa.” Watu wamoja walimuletea Yesu hata watoto wadogo kusudi awaguse. Wanafunzi walipoona vile, wakawakaripia watu wale. Lakini Yesu akawaita na kusema: “Muwaache watoto wadogo wakuje kwangu, wala musiwakataze, kwa maana Ufalme wa Mungu ni wa watu wanaokuwa sawasawa na wao. Kweli ninawaambia: ‘Mutu yeyote asiyekubali Ufalme wa Mungu kama mutoto mudogo, hawezi kuingia katika Ufalme ule hata kidogo.’ ” Mutawala mumoja akamwuliza Yesu: “Mwalimu mwema, nifanye nini kusudi nipate uzima wa milele?” Yesu akamwuliza: “Sababu gani unaniita mwema? Hakuna mutu anayekuwa mwema isipokuwa Mungu peke yake. Unajua jinsi amri zinavyosema kwamba: ‘Usizini, usiue, usiibe, usishuhudie uongo, uwaheshimu baba yako na mama yako.’ ” Yule mutu akamujibu: “Nimetii amri zile zote tangu ujana wangu.” Yesu aliposikia maneno haya, akamwambia: “Ungali unakosewa na kitu kimoja tu: uuzishe vitu vyote unavyokuwa navyo, na uwape wamasikini mali zile, nawe utakuwa na akiba mbinguni. Kisha urudie unifuate!” Lakini mutu yule aliposikia maneno yale, akahuzunika sana kwa sababu alikuwa tajiri sana. Yesu alipoona kwamba amehuzunika sana, akasema: “Kweli ni vigumu sana kwa watajiri kuingia katika Ufalme wa Mungu, lakini ni kwepesi zaidi kwa ngamia kupita katika tundu la sindano kuliko tajiri kuingia katika Ufalme wa Mungu.” Nao waliosikia maneno haya wakasema: “Ni nani basi anayeweza kuokolewa?” Yesu akajibu: “Mambo yasiyoweza kutendeka kwa uwezo wa mwanadamu yanawezekana kwa Mungu.” Basi Petro akamwambia: “Sisi tumeacha vyote tulivyokuwa navyo na kukufuata wewe!” Yesu akawaambia: “Kweli ninawaambia: kama mutu akiacha nyumba yake, muke, wandugu, wazazi, au watoto wake kwa ajili ya Ufalme wa Mungu, atapokea mara mingi zaidi katika wakati wa sasa. Na katika wakati utakaokuja atapokea uzima wa milele.” Halafu Yesu akawatwaa wanafunzi wake kumi na wawili pembeni, akawaambia: “Tunapanda kwenda Yerusalema, na maneno yote yaliyoandikwa na manabii juu ya Mwana wa Mutu yatatimizwa. Maana atatolewa katika mikono ya watu wa mataifa mengine. Watamuchekelea, watamutukana na kumutemea mate. Watamupiga fimbo na kisha watamwua. Lakini kwa siku ya tatu kisha kufa kwake atafufuka!” Wanafunzi wake hawakufahamu maana ya maneno hayo, kwa sababu yalikuwa yamefichwa kwao, nao hawakutambua kama Yesu alisema juu ya nini. Yesu alipokaribia muji Yeriko, mutu mumoja kipofu alikuwa akiikaa pembeni ya njia akiombaomba. Aliposikia kundi la watu wakipita, akauliza juu ya mambo yanayopitika. Wakamwambia kwamba ni Yesu wa Nazareti ndiye anayepita. Basi akalalamika akisema: “Yesu Mwana wa Daudi, unisikilie huruma!” Watu waliotangulia wakamukaripia na kumunyamazisha, lakini alizidi kulalamika, akisema: “Mwana wa Daudi, unisikilie huruma!” Yesu akasimama, akaamuru wamulete kwake. Yule kipofu alipokaribia, Yesu akamwuliza: “Unataka nikufanyie nini?” Akamujibu: “Bwana, ninataka nipate kuona.” Yesu akamwambia: “Upate kuona! Imani yako imekuponyesha.” Na pale pale akapata kuona, na kumufuata Yesu akishukuru Mungu. Na watu wote walipoona jambo hili wakamusifu Mungu. Yesu alipoingia katika muji Yeriko, akapita katikati yake. Kule kulikuwa mutu mumoja jina lake Zakayo aliyekuwa mukubwa wa walipishaji wa kodi, naye alikuwa tajiri. Alitaka kuona Yesu ni nani, lakini kwa vile alivyokuwa mutu mufupi, hakuweza kumwona kwa sababu watu walikuwa wengi. Halafu akatangulia mbio na kupanda juu ya muti wa mukuyu apate kumwona Yesu, kwa sababu Yesu alipaswa kupitia kwenye njia ile. Yesu alipofika kwenye nafasi ile akainua macho na kumwambia: “Zakayo, shuka mbio; kwa maana imenipasa kupanga ndani ya nyumba yako leo.” Zakayo akashuka mbio na kumukaribisha kwa furaha. Watu wote walioona hayo wakaanza kunungunika wakisema: “Amekwenda kupanga kwa mutenda maovu!” Lakini Zakayo akasimama mbele ya Bwana na kumwambia: “Bwana! Ninawapa masikini nusu ya mali zangu, na kama nimetwaa kitu cha mutu kwa kumudanganya, nitamurudishia mara ine sawa na kitu kile.” Yesu akamwambia: “Leo nyumba hii imeokolewa, kwa sababu mutu huyu vilevile ni wa uzao wa Abrahamu. Kwa maana Mwana wa Mutu alikuja kutafuta na kuokoa yule aliyepotea.” Watu walipokuwa wakisikiliza maneno hayo, Yesu akaongeza kuwaambia mufano mumoja, kwa sababu alikuwa karibu na muji Yerusalema, na watu wale walizani kwamba siku za Ufalme wa Mungu zitafika saa ile ile. Basi akasema: “Mutu mumoja mwenye heshima alifunga safari kwenda katika inchi ya mbali kusudi asimikwe kuwa mufalme na kisha arudie. Mbele ya kuondoka kwake akawaita watu kumi kati ya watumishi wake, akamupatia kila mumoja furushi moja ya zahabu na kuwaambia: ‘Mufanye nazo uchuuzi mpaka nitakaporudia.’ Lakini wanainchi wenzake walimuchukia. Kwa hiyo wakatuma wajumbe kumufuata nyuma waende kusema: ‘Hatutaki mutu huyu kuwa mufalme wetu.’ “Lakini yule mutu mwenye heshima alisimikwa kuwa mufalme, na kurudia kwake. Halafu akaamuru wamwitie wale watumishi aliowapatia zahabu kusudi apate kujua kila mumoja amefaidia ngapi. Mutumishi wa kwanza akakuja, akasema: ‘Bwana, furushi moja uliyonipatia imefaidia zingine kumi.’ Naye akamwambia: ‘Ni vizuri wewe mutumishi mwema. Kwa sababu ulikuwa mwaminifu katika jambo dogo, ninakupa utawala juu ya miji kumi.’ Mutumishi wa pili akakuja akasema: ‘Bwana, furushi moja uliyonipatia imefaidia zingine tano.’ Naye akamwambia: ‘Nawe vilevile ninakupa utawala juu ya miji mitano.’ Kisha mutumishi mwingine akakuja akasema: ‘Bwana, furushi yako ndiyo hii. Niliichunga vizuri nikiifunga ndani ya kitambaa, kwa maana nilikuogopa kwa maana wewe ni mutu mugumu. Unatafutia nafasi usipowekea na kuvuna nafasi usipopanda.’ Yule bwana akamujibu: ‘Wewe mutumishi mubaya! Nitakuhukumu kufuatana na maneno yako. Ulijua kama mimi ni mutu mugumu, ninayetafutia nafasi nisipowekea na kuvuna nafasi nisipopanda. Kwa nini basi haukuweka feza yangu katika banki, kusudi siku ya kurudia kwangu ningepata mali yangu pamoja na faida yake?’ Halafu akawaambia wale waliokuwa pale: ‘Mumunyanganye ile furushi moja na kuitoa kwa yule anayekuwa na furushi kumi.’ Wakamwambia: ‘Bwana, amekwisha kuwa na furushi kumi!’ Akawajibu: ‘Ninawaambia kwamba mutu anayekuwa na kitu ataongezewa kingine, lakini mutu asiyekuwa na kitu ataondolewa hata kidogo anachokuwa nacho. Na sasa kwa ngambo ya wale waadui zangu walionikataa mimi kuwa mufalme wao, muwalete hapa na kuwaua mbele yangu.’ ” Kisha kusema maneno hayo, Yesu akatembea mbele ya kundi la watu kwenda Yerusalema. Alipokaribia kufika katika kijiji cha Betefage na cha Betania upande wa mulima wa Mizeituni, Yesu akawatuma wawili kati ya wanafunzi wake, akiwaambia: “Mwende katika kijiji kinachokuwa mbele yenu. Mutakapofika kule, mutaona mwana-punda amefungwa, na hakuna mutu aliyekwisha kupanda juu yake. Mumufungue na kumuleta hapa. Na kama mutu akiwauliza: ‘Kwa sababu gani munamufungua?’, mumwambie: ‘Bwana yuko na lazima ya kumutumia.’ ” Basi wale waliotumwa wakaenda, wakakuta vyote kama vile Yesu alivyowaambia. Walipokuwa wakimufungua, wenyeji wa mwana-punda yule wakawauliza: “Kwa nini munamufungua mwana-punda huyu?” Wakajibu: “Bwana yuko na lazima ya kumutumia.” Wakamuletea Yesu yule mwana-punda, wakatandika nguo zao juu yake na kumupandisha Yesu juu yake. Alipokuwa akiendelea, watu walitandika nguo zao katika njia. Alipokaribia Yerusalema kwenye mutelemuko wa mulima wa Mizeituni, kundi zima la wanafunzi wakafurahi na kuanza kumusifu Mungu kwa sauti kubwa kwa ajili ya miujiza yote waliyoiona. Wakasema: “Abarikiwe mufalme anayekuja kwa jina la Bwana! Amani mbinguni na utukufu kwa Mungu anayekuwa juu!” Kwa hiyo, wamoja kati ya Wafarisayo waliokuwa katika kundi la watu wakamwambia Yesu: “Mwalimu, uwakaripie wanafunzi wako!” Yesu akawajibu: “Ninawaambia ninyi: kama watu hawa wakinyamaza, mawe yatalalamika.” Yesu alipokaribia muji wa Yerusalema, na alipouona, akaulilia, akisema: “Kama wewe vilevile ungejua leo hii kitu kinachoweza kukuletea amani! Lakini sasa kitu hicho kimefichwa, nawe hauwezi kukiona! Kwa maana siku zitakufikia wakati waadui zako watakapokuzunguka kwa vita, watakapojenga ukuta wa kujikingia pembeni yako, na kukusonga pande zote. Watakuharibu kabisa pamoja na wakaaji wako. Hawatakuachia hata jengo moja lisilobomolewa kwa sababu haukutambua wakati Mungu alipokuja kukuokoa.” Halafu Yesu akaingia katika hekalu, akaanza kufukuza wachuuzi na kuwaambia: “Imeandikwa katika Maandiko Matakatifu: ‘Nyumba yangu itakuwa nyumba ya maombi.’ Lakini ninyi munaigeuza kuwa nafasi ya kukutania ya wanyanganyi!” Yesu alikuwa akifundisha kila siku ndani ya hekalu. Lakini wakubwa wa makuhani na walimu wa Sheria pamoja na wakubwa wa watu wakatafuta kumwua. Lakini hawakupata namna ya kumwua, kwa sababu watu wote walimusikiliza kwa uangalifu. Siku moja Yesu alikuwa katika hekalu akiwafundisha watu na kuhubiri Habari Njema. Wakubwa wa makuhani na walimu wa Sheria pamoja na wasimamizi wa watu wakamufikia na kumwuliza: “Utuambie ni kwa mamlaka gani unafanya mambo haya, na ni nani aliyekupa mamlaka yale?” Yesu akawajibu: “Mimi vilevile nitawauliza ulizo hili moja. Muniambie, Yoane alipata mamlaka ya kubatiza kutoka kwa nani? Kwa Mungu au kwa watu?” Nao wakaanza kupiga mafikiri pamoja na kusema: “Kama tukijibu kwamba mamlaka yake yalitoka kwa Mungu, atauliza: ‘Kwa sababu gani basi hamukumwaminia?’ Lakini vilevile hatuwezi kusema kwamba yalitoka kwa watu, kwa maana watu wote watatutupia mawe, kwa sababu wanasadiki kwamba Yoane alikuwa nabii.” Basi wakajibu kwamba hawajui mamlaka yake yalitoka wapi. Yesu akawaambia: “Nami vilevile sitawaambia ninyi ni kwa mamlaka gani ninafanya mambo haya.” Akaendelea kuwaambia watu mufano huu: “Mutu mumoja alipanda shamba la mizabibu. Kisha kupatana kugawanyana mavuno na walimaji wamoja watakaobaki wakitunza shamba lake, akaenda safari katika inchi ingine na kukaa kule kwa muda murefu. Siku za mavuno zilipotimia, akamutuma mutumishi wake mumoja kwa wale walimaji kusudi wamupatie sehemu yake ya mavuno. Lakini wale walimaji wakamupiga na kumurudisha mikono mitupu. Mwenye shamba akatuma tena kwao mutumishi mwingine, lakini wakamupiga vilevile na kumutukana. Kisha wakamurudisha mikono mitupu. Mwenye shamba akatuma tena kwao mutumishi wa tatu, yule naye wakamwumiza na kumutupa inje ya shamba. Halafu yule mwenye shamba akasema: ‘Nitafanya nini? Nitamutuma mwana wangu mupendwa; labda watamuheshimu.’ Lakini wale walimaji walipomwona akikuja, wakasemezana: ‘Musimame! Huyu ndiye atakayerizi shamba hili. Basi tumwue kusudi shamba hili lipate kuwa urizi wetu.’ Halafu wakamukamata wakamwua na kutupa maiti yake inje ya shamba.” Kisha Yesu akauliza: “Basi yule mwenye shamba atawatendea walimaji wale namna gani? Atakuja na kuwaua wale walimaji. Na kisha atawapatia walimaji wengine shamba lile.” Watu waliposikia maneno hayo, wakasema: “Isitufikie vile hata kidogo.” Lakini Yesu akawaangalia na kuwauliza: “Maana ya Maandiko haya Matakatifu ni gani? ‘Jiwe lililokataliwa na wajengaji, limekuwa sasa jiwe kubwa la musingi.’ Kila mutu atakayeanguka juu ya jiwe lile, atavunjika na yule litakayemwangukia, litamuponda.” Saa ile ile wakubwa wa makuhani na walimu wa Sheria wakatafuta kumukamata, kwa sababu walitambua kwamba alisema mufano huo juu yao. Basi wakaanza kumuvizia Yesu, wakatuma wapelelezi waliojifanya kuwa kama watu wazuri kusudi wamunase katika masemi. Na kwa njia ile waweze kumutoa katika mikono ya watawala wa inchi. Wale wapelelezi wakamwuliza: “Mwalimu, tunajua kwamba unasema na kufundisha maneno ya kweli. Vilevile wewe hauangalii cheo cha mutu, lakini unafundisha juu ya namna ya kuishi ambayo Mungu anaamuru kufuata. Utuambie basi, Sheria inaturuhusu kulipa kodi kwa Mufalme wa Roma au hapana?” Lakini kwa kuwa Yesu alitambua udanganyifu wao, akawaambia: “Munionyeshe kikoroti kimoja cha feza.” Kisha akawauliza: “Sura hii na jina hili linaloandikwa hapa ni vya nani?” Nao wakajibu: “Ni vya Mufalme wa Roma.” Halafu Yesu akawaambia: “Basi mumupe Mufalme wa Roma vinavyokuwa vyake, na Mungu vinavyokuwa vyake.” Basi watu wale hawakuweza kumunasa katika neno lolote mbele ya watu, lakini wakashangaa na jibu lake, nao wakanyamaza. Wasadukayo wamoja (ndio wale watu wanaosema kwamba wafu hawatafufuka) wakamufikia Yesu na kumwuliza: “Mwalimu, Musa alituamuru: Mutu akiwa na ndugu yake, naye akikufa na kuacha muke wake bila mutoto, yule ndugu yake anapaswa kumwoa yule mujane na kumuzalia ndugu yake marehemu watoto. Basi kulikuwa wandugu saba. Wa kwanza alioa mwanamuke, lakini mutu yule akakufa bila kuacha mutoto. Ndugu wa pili akaoa yule mujane, akakufa vilevile bila kuacha mutoto. Na ikakuwa vile kwa ndugu wa tatu na hata kwa wote saba. Wote wakakufa bila kuacha mutoto. Na kwa mwisho, yule mwanamuke akakufa vilevile. Sasa, siku wafu watakapofufuka, muke yule atakuwa wa nani, kwa maana wote saba walikuwa wamemwoa?” Yesu akawajibu: “Watu wa nyakati hizi wanaoa na kuolewa. Lakini wale watakaohesabiwa kwamba wanastahili kufufuliwa na kuishi katika nyakati zile zitakazokuja, hawataoa wala kuolewa. Na zaidi ya ile hawataweza kufa tena, kwa sababu wataishi sawa vile wamalaika wanavyoishi. Nao watakuwa watoto wa Mungu, kwa sababu wamefufuliwa. Musa alionyesha waziwazi kwamba wafu watafufuka. Katika maandiko yake yanayosema juu ya kichaka kilichowaka moto, yeye anamutaja Bwana kuwa ni ‘Mungu wa Abrahamu, Mungu wa Isaka na Mungu wa Yakobo.’ Yeye si Mungu wa wafu, lakini ni Mungu wa wanaokuwa wazima; maana mbele yake wote wanaishi.” Walimu wamoja wa Sheria wakasema: “Mwalimu, umejibu vizuri!” Na hakuna mutu aliyesubutu tena kumwuliza maneno mengine. Yesu akaongeza kuwaambia: “Namna gani wanaweza kusema kwamba Kristo ni Mwana wa Daudi? Daudi yeye mwenyewe alisema katika kitabu cha Zaburi: ‘Bwana wetu Mungu alimwambia Bwana wangu: Ikaa na mamlaka kwa kuume kwangu mpaka nitakapoweka waadui zako chini ya miguu yako.’ Daudi anamwita Kristo ‘Bwana’; namna gani basi Kristo anaweza kuwa Mwana wake?” Watu wote walipokuwa wakimusikiliza Yesu, yeye akawaambia wanafunzi wake: “Mujiepushe na walimu wa Sheria wanaopenda kujitembeza, wakivaa kanzu ndefu na kusalimiwa kwa heshima kwenye nafasi za makutano. Wanapenda vilevile kuikaa katika viti vya mbele ndani ya nyumba za kuabudia, na kwenye nafasi za heshima katika karamu. Wananyanganya mali ya wajane na kuomba maombi marefu kusudi waonekane mbele ya watu. Kwa sababu hii watahukumiwa vikali sana!” Yesu alipoinua macho, akawaona watajiri wakitia sadaka ndani ya sanduku ya sadaka za hekalu. Akaona vilevile mujane mumoja masikini akitia ndani ya ile sanduku vikoroti viwili vidogo sana. Basi akasema: “Kweli ninawaambia kwamba mujane huyu masikini ametoa mingi zaidi kuliko watu wote wengine. Kwa maana hawa wengine wote walitoa sehemu ya mali wasiyokuwa nayo lazima. Lakini yeye ametoa kwa umasikini wake mali yote aliyokuwa nayo kwa kuishi.” Wamoja kati ya wanafunzi wa Yesu walikuwa wakizungumuza juu ya hekalu, wakisema juu ya majengo yake mazuri ya mawe na juu ya vitu vingine vizuri watu walivyovitoa sadaka kwa Mungu. Lakini Yesu akasema: “Kutakuwa siku vitu hivi munavyoona vitabomolewa, wala hakutabaki hata jiwe moja juu ya lingine.” Halafu wakamwuliza: “Mwalimu, mambo hayo unayotoka kusema yatakuwa wakati gani? Na ni kitambulisho gani kitakachoonyesha kwamba yanataka kutimia?” Yesu akawajibu: “Muangalie vizuri, musidanganywe. Watu wengi watakuja wakijiita kwa jina langu, wakisema kwamba wao ndio Kristo, nao wakati umetimia. Ingawa vile, musiwafuate. Musiogope wakati mutakaposikia habari za vita na za mapinduzi. Sherti mambo hayo yatukie kwanza, lakini haionyeshi kwamba mwisho wa dunia unatimia palepale.” Kisha Yesu akaongeza kusema: “Taifa litapigana na taifa, nao ufalme utapigana na ufalme. Kutakuwa tetemeko kubwa la inchi. Vilevile kutakuwa njaa na magonjwa makali kwenye nafasi mbalimbali. Zaidi ya ile kutakuwa mambo ya kuogopesha na vitambulisho vya ajabu toka mbinguni. Lakini mbele mambo hayo yote yatokee, mutakamatwa na kuteswa. Watawapeleka kwenda kuhukumiwa katika nyumba za kuabudia na kuwatia katika vifungo. Vilevile mutapelekwa mbele ya wafalme na ya wakubwa kwa ajili ya jina langu, kusudi mutoe ushuhuda wangu mbele yao. Basi mukusudie ndani ya moyo kwamba hamutajihangaisha mbele ya wakati kwa kutafuta kujua namna mutakavyojitetea. Kwa maana mimi mwenyewe nitawapa masemi na hekima hata waadui zenu hawataweza kuyapinga wala kuyakataa. Mutatolewa hata na wazazi wenu, wandugu zenu, na watu wa jamaa zenu pamoja na warafiki zenu. Nao watawaua wamoja kati yenu. Watu wote watawachukia kwa ajili ya jina langu. Lakini hata unywele mumoja wa kichwa chenu hautapotea. Lakini muendelee kuvumilia, maana kwa njia ile mutaokoa uzima wenu.” “Wakati mutakapoona muji wa Yerusalema umezungukwa na waaskari, mujue kwamba uharibifu wake unakaribia. Basi wale watakaokuwa Yudea, wakimbilie kwa milima, na wale watakaokuwa Yerusalema watoke ndani yake, nao wale watakaokutiwa katika mashamba wasiingie ndani ya muji. Kwa maana siku zile zitakuwa siku za azabu ya Mungu, kusudi mambo yote yaliyoandikwa katika Maandiko Matakatifu yatimie. Wanawake wenye mimba na wenye kunyonyesha watapata hasara katika siku zile! Kwa maana kutakuwa taabu kubwa katika inchi, na Mungu ataonyesha kasirani yake juu ya watu wa taifa hili. Wamoja watauawa kwa vita na watapelekwa kuwa wafungwa katika inchi za mataifa yote. Vilevile mataifa mengine yatautawala Yerusalema mpaka nyakati zao za kuutawala zitakapokwisha.” “Vitambulisho vitaonekana katika jua, mwezi na nyota. Na hapa katika dunia mataifa yatakuwa na uchungu, na kushikwa na wasiwasi kwa ajili ya mungurumo na musukosuko wa bahari. Watu watazimia kwa ajili ya hofu, wakingojea mambo yatakayotokea katika dunia, kwa maana vyote vyenye nguvu katika mbingu vitatikiswa. Halafu wakati ule Mwana wa Mutu ataonekana akikuja katikati ya mawingu, kwa uwezo mwingi na kwa utukufu. Mambo hayo yatakapoanza kutokea, muinue kichwa na kusimama na nguvu, kwa sababu wakati wa kukombolewa kwenu umekaribia.” Kisha Yesu akawaambia wanafunzi wake mufano huu: “Muchunguze vizuri muti wa tini na miti yote mingine. Munapoona kwamba majani yao yanaanza kuchipuka, munatambua wenyewe kwamba wakati wa jua kali unakaribia. Vilevile wakati mutakapoona mambo hayo niliyotoka kutaja yanatokea, mujue kwamba Ufalme wa Mungu unakaribia. “Kweli ninawaambia: hiki kizazi hakitapita mbele ya kutimia kwa mambo yote. Mbingu na dunia vitatoweka, lakini maneno yangu hayatabadilika hata kidogo. “Mujilinde vizuri, kusudi musilemewe na kutafuta kula ulafi, kulewa na kusumbukia maisha. Kama si vile, Siku ile ya kurudia kwa Kristo itawafikia kwa rafla sawa mutego. Kwa maana Siku ile itawafikia watu wote wa dunia. Basi mukeshe na kuomba kila wakati, kusudi mupate nguvu ya kuepuka mambo hayo yote yatakayotokea, nanyi mupate kuweza kusimama mbele ya Mwana wa Mutu.” Yesu alikuwa akipitisha muchana katika hekalu akihubiri, na usiku alikuwa akienda kulala kwenye mulima wa Mizeituni. Watu wote walikuwa wakimufikia asubui mapema katika hekalu, kusudi wamusikilize. Sikukuu ya Mukate Usiotiwa Chachu, inayoitwa Pasaka, ilikaribia. Wakubwa wa makuhani na walimu wa Sheria walitafuta njia ya kumwua Yesu, lakini waliogopa watu. Basi Shetani akamwingia Yuda, yule anayeitwa Iskariota, aliyekuwa mumoja wa wanafunzi kumi na wawili. Halafu Yuda akaenda kusikilizana na wakubwa wa makuhani na wakubwa wa walinzi wa hekalu juu ya namna ya kumutoa Yesu kwao. Wakafurahi sana, wakapatana kumupa feza. Yuda akakubali na kuanza kutafuta wakati unaokuwa muzuri kwa kumutoa Yesu kwao, kwa uficho pasipo watu kujua. Siku ya karamu ya Mukate Usiotiwa Chachu, ndiyo siku ile walipaswa kuchinja kondoo waliotayarishwa kwa ajili ya Pasaka ikatimia. Yesu akawatuma Petro na Yoane, akisema: “Mwende mututayarishie chakula cha karamu ya Pasaka.” Wakamwuliza: “Ni wapi unapotaka tuende tukitayarishie?” Akawajibu: “Mutakapoingia katika muji, mutakutana mutu mumoja anayebeba mutungi wenye maji. Mumufuate mutu yule katika nyumba atakamoingia, mumwambie mwenye nyumba: ‘Mwalimu anakuuliza kwamba ni wapi kunapokuwa chumba cha kukulia karamu ya Pasaka pamoja na wanafunzi wake.’ Naye atawaonyesha chumba kikubwa cha gorofi kilichokwisha kupangwa vizuri. Ni mule mutakapotayarishia karamu.” Wakaenda na kukuta vitu vyote sawa vile Yesu alivyowaambia. Nao wakatayarisha karamu ya Pasaka. Saa ilipotimia, Yesu akaikaa kula chakula pamoja na wanafunzi wake. Akawaambia: “Nimetamani sana kula karamu hii ya Pasaka pamoja nanyi mbele ya kuteswa kwangu! Kwa maana ninawaambia, sitakula tena karamu hii ya Pasaka mpaka siku ile nitakapokula ile yenye kukamilika katika Ufalme wa Mungu.” Kisha Yesu akatwaa kikombe, akakibariki na kusema: “Mutwae kikombe hiki na mukigawanye kati yenu. Kwa maana ninawaambia kwamba tangia sasa sitakunywa tena divai mpaka Ufalme wa Mungu utakapokuja.” Halafu akatwaa mukate, akaubariki, kisha akaumega na kuwapa akisema: “Huu ni mwili wangu [unaotolewa kwa ajili yenu. Mufanye hivi kwa kunikumbuka.” Vilevile kisha kula akatwaa kikombe na kuwapa akisema: “Kikombe hiki ni agano jipya la Mungu, linalohakikishwa kwa njia ya damu yangu.] “Lakini muangalie: yule anayenitoa anachangia chakula pamoja nami. Kwa maana Mwana wa Mutu atakufa sawa vile ilivyokusudiwa na Mungu; lakini ole kwa mutu yule atakayemutoa!” Basi wakaanza kuulizana wao kwa wao ni nani kati yao atakayefanya jambo lile. Kulitokea ubishi kati ya wanafunzi wa kujua nani anayekuwa mukubwa kati yao. Yesu akawaambia: “Wafalme wa mataifa wanawatawala watu wao kwa nguvu; na wale wenye mamlaka juu yao wanajiita ‘Watenda mema.’ Lakini isikuwe hivi katikati yenu. Lakini yule anayekuwa mukubwa kati yenu sherti akuwe mudogo zaidi, na yule anayekuwa mwongozi sherti akuwe kama mutumishi. Kwa maana, ni nani anayekuwa mukubwa; yule anayeikaa kwa kula chakula au yule anayemushugulikia? Hakika ni yule anayeikaa kwa kula chakula. Ingawa vile mimi niko hapa katikati yenu kama mwenye kushugulika! “Ninyi ndio muliokuwa pamoja nami katika majaribu yangu. Nami ninawawekea ninyi ufalme kama vile Baba yangu alivyoniwekea mimi, kusudi mupate kula na kunywa pamoja nami katika ufalme wangu. Mutaikaa vilevile juu ya viti vya kifalme, kwa kuhukumu makabila kumi na mawili ya Waisraeli.” “Simoni, Simoni! Sikiliza: Shetani ameachiliwa wakati wa kuwajaribu na kuwatenga kabisa. Lakini mimi nimekuombea, kusudi usipungukiwe na imani. Nawe utakaponirudilia tena, uwatie wandugu zako moyo.” Petro akamwambia: “Bwana, mimi niko tayari kufungwa pamoja nawe na hata kufa pamoja nawe.” Yesu akamujibu: “Ninakuambia wewe Petro kwamba leo, mbele jogoo hajawika utakuwa umenikana mara tatu kuwa haunijui.” Halafu Yesu akawauliza wanafunzi wake: “Nilipowatuma pasipo kubeba feza, wala mufuko, wala viatu, mulikosewa na kitu gani?” Wakamujibu: “Hakuna.” Naye akawaambia: “Lakini sasa, yule anayekuwa na feza azitwae, na anayekuwa na mufuko autwae vilevile. Na yeyote asiyekuwa na upanga, auzishe nguo yake apate kuununua. Kwa maana ninawaambia, ni lazima yatimie kwangu maneno haya yaliyoandikwa katika Maandiko Matakatifu: ‘Naye alihesabiwa pamoja na watenda maovu.’ Kwa sababu yanayonielekea mimi yanafikia kwa mwisho wake.” Wanafunzi wakasema: “Bwana, angalia, tuna panga mbili hapa.” Akajibu: “Basi, inatosha.” Yesu akatoka na kwenda kwa mulima wa Mizeituni kama ilivyokuwa desturi yake. Na wanafunzi wake wakamufuata. Alipofika kwenye nafasi ile, akawaambia: “Muombe kusudi musianguke katika majaribu.” Kisha akajitenga nao na kuenda kwenye hatua ya mutu kuweza kutupa jiwe, akapiga magoti, akaomba akisema: “Baba, kama ukitaka, ninakuomba uniondolee mbali kikombe cha mateso. Lakini isikuwe mapenzi yangu ndiyo yafanyike, lakini yako.” [ Halafu malaika toka mbinguni alimutokea kwa kumutia moyo. Yesu alikuwa katika uchungu mukubwa, akazidi kuomba kwa bidii. Jasho iliyomutoka ikakuwa kama matone ya damu yaliyokuwa yakitiririka mpaka chini.] Kisha kuomba, alirudia pahali alipoacha wanafunzi wake, akawakuta wamelala kwa sababu walikuwa na huzuni. Akawaambia: “Sasa, ninyi munalala? Muamuke na muombe, kusudi musianguke katika majaribu.” Yesu alipokuwa hajamaliza kusema, kundi la watu wakafika, wakiongozwa na Yuda, mumoja wa wanafunzi kumi na wawili. Akamujongelea Yesu kusudi amubusu. Lakini Yesu akamwuliza: “Yuda, unamutoa Mwana wa Mutu kwa kumubusu?” Wale wanafunzi wa Yesu walipoona mambo yatakayotendeka, wakamwuliza: “Bwana, tuwakate kwa panga?” Na mumoja wao akamupiga mutumishi wa Kuhani Mukubwa upanga na kumukata sikio la kuume. Lakini Yesu akasema: “Mwache, inatosha!” Akagusa sikio la mutu yule, na kumuponyesha. Halafu Yesu akawaambia wakubwa wa makuhani, wakubwa wa walinzi wa hekalu na wazee waliokuja kumukamata: “Mumekuja na panga na magongo kama vile wanavyokwenda kukamata munyanganyi? Siku zote nilipokuwa pamoja nanyi katika hekalu, ninyi hamukunikamata. Lakini hii ni saa yenu; saa ya utawala wa bwana wa giza.” Walipokwisha kumukamata, wakamupeleka katika nyumba ya Kuhani Mukubwa. Petro akamufuata Yesu kwa mbali. Wakakonga moto katikati ya kiwanja na kuikaa, na Petro akakuja kuota moto pamoja nao. Mutumishi mumoja mwanamuke alipomwona Petro akiikaa karibu na moto, akamukazia macho na kusema: “Mutu huyu vilevile alikuwa pamoja naye.” Lakini Petro akakana, akisema: “Ewe mama, mimi simujui!” Nyuma kidogo mutu mwingine akamwona, na akasema: “Wewe vilevile ni mumoja wao!” Lakini Petro akamujibu mutu yule: “Mimi si mumoja wao.” Kisha muda wa karibu saa moja, mutu mwingine akatia mukazo akisema: “Hakika, mutu huyu alikuwa pamoja naye, kwa sababu yeye ni wa Galilaya.” Lakini Petro akasema: “Sijui mambo unayoyasema.” Wakati ule alipokuwa angali akisema, jogoo akawika. Bwana akageuka na kumwangalia Petro. Petro akakumbuka maneno yale Bwana aliyomwambia kwamba mbele jogoo hajawika atakuwa amemukana mara tatu. Basi akatoka inje, akalia kwa uchungu sana. Wale watu waliokuwa wakimuchunga Yesu walimuchekelea na kumupiga. Walimufunika uso kwa kitambaa na kumwuliza: “Tambua sasa, ni nani aliyekupiga?” Nao walimutusi kwa maneno mengine mengi. Usiku ulipokucha, wazee wa Wayuda, wakubwa wa makuhani na walimu wa Sheria, wakakusanyika. Wakamuleta Yesu mbele ya Baraza yao Kubwa, na kumwuliza: “Kama wewe ni Kristo, utuambie.” Akawajibu: “Kama ninawaambia, hamutanisadiki, na kama ninawauliza ulizo, hamutanijibu. Lakini zaidi ya hiyo Mwana wa Mutu ataikaa na mamlaka karibu na Mungu Mwenye Uwezo.” Wote wakamwuliza: “Basi, wewe ni Mwana wa Mungu?” Yesu akawajibu: “Ninyi munasema kwamba mimi ndiye.” Halafu wakasema: “Hatuhitaji tena ushuhuda wowote juu yake. Kwa maana tunatoka kusikia maneno aliyosema!” Kisha watu wote wa Baraza Kubwa wakasimama, wakamupeleka Yesu mbele ya Pilato. Wakaanza kumushitaki, wakisema: “Tulimukuta mutu huyu akiwashawishi watu wa taifa letu kufanya uasi. Yeye alikuwa akiwaambia kwamba wasilipe kodi kwa Mufalme wa Roma. Na zaidi ya hii anasema kwamba yeye ndiye Kristo, Mufalme aliyengojewa.” Basi Pilato akamwuliza Yesu: “Wewe ndiwe mufalme wa Wayuda?” Yesu akamujibu: “Ni wewe ndiwe umesema.” Halafu Pilato akawaambia wakubwa wa makuhani na kundi la watu: “Mimi sioni hata sababu moja ya kumuhukumu mutu huyu.” Lakini wakazidi kusema kwa nguvu: “Kwa njia ya mafundisho yake anawashawishi watu kufanya uasi katika Yudea yote. Alianzia Galilaya na sasa amefika hapa.” Wakati Pilato aliposikia maneno hayo, akauliza: “Mutu huyu ni wa Galilaya?” Naye alipojua kwamba Yesu alikuwa mutu wa jimbo lililokuwa chini ya utawala wa Herode, akamutuma kwa Herode, kwa maana alikuwa Yerusalema siku zile. Herode alipomwona Yesu, akafurahi sana. Tangu siku nyingi alitamani kumwona kwa sababu alikuwa amesikia habari zake, naye alitumaini kuona kitambulisho kutoka kwake. Akamwuliza Yesu maneno mengi, lakini yeye hakumujibu neno. Wakubwa wa makuhani na walimu wa Sheria waliokuwa pale wakatoa mashitaki makubwa sana juu ya Yesu. Basi Herode na waaskari wake wakamuchekelea Yesu na kumuzarau. Wakamuvalisha nguo zinazokuwa sawa za mufalme na kumurudisha kwa Pilato. Siku ile Herode na Pilato waliokuwa waadui tangu zamani, wakageuka kuwa warafiki. Basi Pilato akafanya mukutano wa wakubwa wa makuhani, nao wasimamizi wa watu pamoja na watu wao. Akawaambia: “Mumeniletea mutu huyu mukisema kwamba anashawishi watu kufanya uasi. Basi nimemwuliza mbele yenu juu ya maneno yale, lakini sikumwona na kosa lolote ninyi munalomushitakia. Hata Herode vilevile hakumwona na kosa; na ni kwa sababu hii amemurudisha kwetu. Mutu huyu hakufanya hata kosa moja linalomustahili kuhukumiwa kufa. Basi nitaamuru apigwe fimbo, na kisha nitamufungua.” [ Kila sikukuu ya Pasaka, Pilato alipaswa kuwafungulia watu mufungwa mumoja.] Lakini wote pamoja wakapiga kelele wakisema: “Umwue mutu huyu na utufungulie Baraba!” (Baraba alikuwa amefungwa kwa ajili ya fujo iliyofanyika katika muji na kwa ajili ya kuua watu.) Kufuatana na vile Pilato alivyotaka kumufungua Yesu, yeye akasema tena na watu. Lakini wakapiga tena kelele, wakisema: “Umutundike juu ya musalaba! Umutundike juu ya musalaba!” Pilato akawaambia kwa mara ya tatu: “Alifanya ubaya gani? Mimi sikumwona na hata kosa moja linalomustahili kuhukumiwa kufa. Nitaamuru apigwe fimbo, na kisha nitamufungua.” Lakini wakaendelea kupiga kelele kubwa wakiomba Yesu atundikwe juu ya musalaba. Na kwa mwisho akashindwa kwa sababu ya makelele yao. Halafu akakata shauri la kuwatendea sawa walivyotaka. Akamufungua yule mutu waliyetaka, aliyefungwa kwa ajili ya kuleta fujo na kuua watu, na kumutoa Yesu kwao kusudi wamutendee vile walivyotaka. Nao walipokuwa wakimupeleka Yesu kwenda kutundikwa, wakakutana na mutu mumoja aliyeitwa Simoni, wa inchi ya Kurene, aliyekuwa akitoka kwenye vijiji. Wakamulazimisha abebe musalaba wa Yesu na kumufuata nyuma. Kundi kubwa la watu walimufuata. Kati yao kulikuwa wanawake waliokuwa wakijipigapiga kwenye kifua kwa huzuni na kumulilia. Yesu akawageukia na kuwaambia: “Ninyi wanawake wa Yerusalema, musinililie mimi, lakini mujililie ninyi wenyewe pamoja na watoto wenu. Kwa maana siku zitakuja wakati watu watakaposema: ‘Heri wanawake wanaokuwa tasa, wale waliokosa kuzaa na kunyonyesha!’ Wakati ule watu wataanza kuiambia milima ‘Mutuangukie’, navyo vilima ‘Mutufunike!’ Kwa maana wakifanya hivi kwangu mimi ninayekuwa kama muti mubichi, basi watafanya nini kwenu munaokuwa kama muti unaokauka?” Kulikuwa watu wengine wawili, watenda maovu; walipelekwa pamoja na Yesu kwa kutundikwa. Walipowafikisha kwenye pahali palipoitwa “Kilima cha Mufupa wa Kichwa,” wakamutundika Yesu juu ya musalaba. Vilevile walitundika wale watenda maovu, mumoja kwa upande wa kuume wa Yesu na mwingine kwa upande wa kushoto. Halafu Yesu akasema: “Baba uwasamehe, kwa maana hawajui jambo wanalofanya.” Waaskari wakagawanya nguo zake kwa kuzipigia kura. Watu walisimama pale wakiangalia. Nao wakubwa wa Wayuda walimusimanga Yesu, wakisema: “Aliokoa watu wengine, sasa ajiokoe yeye mwenyewe ikiwa yeye ndiye Masiya, yule aliyechaguliwa na Mungu.” Waaskari vilevile walimuzarau, wakamupelekea divai yenye kuchacha na kumwambia: “Kama wewe ni mufalme wa Wayuda, ujiokoe wewe mwenyewe!” Na mashitaki haya yalikuwa yameandikwa juu ya musalaba wake: “Huyu ndiye Mufalme wa Wayuda.” Mumoja wa wale watenda maovu wawili waliotundikwa juu ya musalaba alimutukana, akisema: “Si wewe ndiwe Kristo? Basi ujiokoe wewe mwenyewe na kutuokoa sisi vilevile.” Lakini mwenzake akamukaripia, akisema: “Wewe haumwogopi Mungu hata kidogo ingawa unapata azabu ile ile? Sisi tunahukumiwa kwa haki, kwa maana tunaazibiwa kufuatana na matendo yetu mabaya. Lakini mutu huyu hakufanya ubaya wowote.” Na akaongeza kusema: “Ee Yesu, usinisahau wakati utakapokuja katika ufalme wako!” Yesu akamujibu: “Kweli ninakuambia wewe: leo hii utakuwa pamoja nami katika Paradizo.” Yesu akalalamika kwa sauti kubwa akisema: “Baba, ninatoa uzima wangu kwako.” Kisha kusema maneno haya, akakata roho. Mukubwa wa waaskari alipoona mambo yale yaliyotokea, akamusifu Mungu, akisema: “Hakika mutu huyu alikuwa mwenye haki!” Nalo kundi la watu waliofika kuangalia mambo yale, wakaona yote yaliyotokea. Kwa hiyo, wakarudia wakijipigapiga kwenye kifua kwa huzuni. Na wote waliojuana sana naye, na hata wanawake waliomufuata tangia Galilaya, walisimama kwa mbali wakiangalia mambo hayo. Yosefu alienda kwa Pilato kwa kumwomba maiti ya Yesu. Alipokwisha kuishusha toka juu ya musalaba, akaifungafunga na vitambaa na kuiweka ndani ya kaburi lililochimbwa katika jiwe. (Ndani ya kaburi lile mulikuwa bado hamujazikwa mutu.) Siku ile ilikuwa ya matayarisho ya siku ya Sabato iliyokuwa karibu kuanza. Wale wanawake waliokuja na Yesu tangia Galilaya walimufuata Yosefu, wakaona kaburi na namna maiti ya Yesu ilivyowekwa mule. Kisha wakarudia kwao kutengeneza mafuta na marasi ya kupakaa maiti. Siku ya Sabato wakapumzika kama Sheria ilivyoamuru. Siku ya kwanza ya juma, asubui mapema, wale wanawake wakaenda kwenye kaburi, nao walibeba yale mafuta waliyotengeneza. Walipofika, wakakuta jiwe kubwa limekwisha kusukumwa pembeni ya kiingilio cha kaburi. Lakini walipoingia ndani ya kaburi hawakuona maiti ya Bwana Yesu. Walipokuwa wakifazaika kwa ajili ya jambo hili, mara moja watu wawili waliovaa nguo zenye kungaa wakawatokea. Kwa sababu ya woga, wale wanawake wakainama uso mpaka chini. Lakini wale watu wakawaambia: “Kwa sababu gani munamutafuta yule anayekuwa muzima kati ya waliokufa? Yeye hayuko hapa; amefufuka! Mukumbuke jinsi alivyowaambia wakati alipokuwa angali Galilaya. Aliwaambia kwamba Mwana wa Mutu anapaswa kutolewa katika mikono ya wenye zambi, na kutundikwa juu ya musalaba, lakini kwa siku ya tatu kisha kufa, atafufuka.” Halafu wakakumbuka maneno yale Yesu aliyosema. Waliporudia toka kwenye kaburi, wakapasha habari ile kwa wanafunzi kumi na mumoja na kwa wafuasi wengine wote wa Yesu. Na hawa ndio waliowapasha habari ile kwa mitume: Maria wa Magdala, Yoana na Maria mama ya Yakobo. Kulikuwa vilevile wanawake wengine pamoja nao. Lakini mitume hawakusadiki maneno ya wale wanawake, waliwaza kwamba ni ya bure. Lakini Petro alisimama, akaenda mbio mpaka kwenye kaburi. Alipoinama kuchungulia ndani yake, akaona tu vile vitambaa. Kisha akarudia kwake, akishangaa kwa ajili ya mambo yaliyotokea. Siku ile ile, wawili kati ya wanafunzi walikuwa wakienda kwenye kijiji cha Emau, kilichokuwa kwa umbali wa kilometre kumi na moja kutoka Yerusalema. Walikuwa wakiongea juu ya mambo yote yaliyotokea. Walipokuwa wakiongea na kuulizana, Yesu mwenyewe akafika karibu nao, akaendelea kutembea pamoja nao, lakini macho yao yalizuizwa kumutambua. Yesu akawauliza: “Ni maneno gani haya munayosumulia hapa katika njia.” Nao wakasimama, wakiwa wanahuzunika. Na mumoja wao, aliyeitwa Kleopa, akamujibu: “Kati ya wageni wanaokaa Yerusalema ni wewe tu usiyejua mambo yaliyotokea kule katika siku hizi?” Naye akawauliza: “Ni mambo gani?” Nao wakamujibu: “Haujui mambo yaliyomupata Yesu wa Nazareti? Yeye alishuhudiwa na Mungu na watu wote kwamba alikuwa nabii mwenye uwezo katika mambo aliyofanya na kusema. Wakubwa wa makuhani na wasimamizi wetu walimutoa kusudi ahukumiwe kufa, nao wamemutundika juu ya musalaba. Sisi tulikuwa na tumaini kwamba yeye ndiye atakayekomboa Waisraeli. Lakini sasa, leo ni siku ya tatu tangu mambo hayo yalipofanyika. Zaidi ya hiyo wanawake wamoja wa kundi letu walitushitusha. Walienda kwenye kaburi asubui mapema, lakini hawakuona maiti yake. Basi wakarudia kutuelezea kwamba wamalaika waliwatokea na kuwaambia kwamba yeye ni muzima. Halafu wamoja kati yetu walienda kwenye kaburi, nao wakakuta mambo yote ni sawa na vile wale wanawake walivyosema, lakini hawakumwona.” Basi Yesu akawaambia: “Enyi wajinga na wenye mioyo mizito kwa kuamini maneno yote manabii waliyosema! Haikumupasa Kristo ateswe kama vile na aingie kwenye nafasi atakapotukuzwa?” Kisha akawaelezea maneno yaliyoandikwa juu yake katika Maandiko Matakatifu yote, akianza toka vitabu vya Musa na kuendelea katika vitabu vya manabii wote. Nao walipofika karibu na kile kijiji ambamo walikuwa wakienda, Yesu akaendelea mbele, akiwa sawa mwenye kuwaacha. Lakini wakamusihi sana abakie pamoja nao, kwa maana ilikuwa magaribi na giza lilitaka kuingia. Basi akaingia ndani ya nyumba kubakia pamoja nao. Alipokuwa akiikaa kula chakula pamoja nao, akatwaa mukate na kuubariki. Kisha akaumega na kuwapatia. Halafu, macho yao yakafumbuliwa, wakamutambua. Lakini yeye akatoweka, nao hawakumwona tena. Basi wakasemezana: “Mioyo yetu ilichangamuka sana wakati alipokuwa akisimulia nasi katika njia na kutuelezea Maandiko Matakatifu.” Wakaondoka saa ile ile, na kurudia Yerusalema. Kule wakakuta wale mitume kumi na mumoja wamekusanyika pamoja na watu wengine wa kundi lao. Hao waliokusanyika wakawaambia: “Hakika Bwana amefufuka, na amemutokea Simoni!” Nao vilevile wakawaelezea mambo yote yaliyotokea katika njia na namna walivyomutambua Yesu wakati alipomega mukate. Walipokuwa hawajamaliza kuwaelezea mambo hayo, mara moja Yesu mwenyewe akasimama katikati yao, na kuwaambia: “Amani kwenu!” Wakashituka na kuogopa, wakizani kwamba wameona muzimu. Lakini Yesu akawaambia: “Kwa sababu gani munafazaika na kuwa na mashaka? Muangalie mikono yangu na miguu yangu, kusudi mupate kutambua kwamba ni mimi. Muniguse, muone, kwa maana muzimu hana mwili wala mifupa kama hivi munavyoniona kuwa navyo.” Alipokwisha kusema vile, akawaonyesha mikono na miguu yake. Nao walipokuwa hawajasadiki bado kwa sababu ya furaha na mushangao, akawauliza: “Muko na chakula chochote hapa?” Wakamupa kipande cha samaki iliyochomwa. Akakitwaa na kukikula mbele yao. Kisha akawaambia: “Haya ndiyo maneno niliyowaambia wakati nilipokuwa ningali pamoja nanyi, kwamba sherti yatimizwe maneno yote yaliyoandikwa juu yangu katika Sheria ya Musa, katika maandiko ya manabii na katika Zaburi.” Halafu akawafungua akili kusudi wapate kufahamu Maandiko Matakatifu akiwaambia: “Imeandikwa katika Maandiko Matakatifu kwamba Kristo atateswa na kufufuka kwa siku ya tatu kisha kufa kwake. Iliandikwa vilevile kwamba kwa jina lake watahubiri mataifa yote, kuanzia Yerusalema, kusudi wageuke toka katika zambi na wapate kusamehewa. Na ninyi ndio mutakaotoa ushuhuda juu ya maneno haya. Na mimi mwenyewe nitawatumia zawadi ile Baba yangu aliyoahidi ishuke juu yenu. Lakini mungojee kule Yerusalema mpaka mutakapojazwa uwezo kutoka juu.” Kisha Yesu akatoka nao katika muji na kwenda karibu na kijiji cha Betania na pale akainua mikono yake juu na kuwabariki. Alipokuwa akiwabariki akajitenga nao na kunyanyuliwa mbinguni. Nao walipokwisha kumwabudu, wakarudia Yerusalema wakifurahi sana. Na siku zote walikuwa ndani ya hekalu wakimusifu Mungu. Kwa mwanzo, Neno alikuwa yuko, naye Neno alikuwa pamoja na Mungu, naye Neno alikuwa Mungu. Kwa mwanzo Neno alikuwa pamoja na Mungu. Vitu vyote viliumbwa kwa njia yake, wala hakuna hata kitu kimoja kilichoumbwa pasipo yeye. Yeye alikuwa chemichemi ya uzima, na uzima huu ulikuwa mwangaza kwa watu. Mwangaza ule uliangaza katika giza, wala giza halikuuzimisha. Kulitokea mutu aliyetumwa na Mungu, jina lake Yoane. Alikuja kushuhudia ule mwangaza kusudi watu wote wapate kuamini kwa njia yake. Yeye mwenyewe hakukuwa mwangaza ule, lakini alikuja tu kuushuhudia. Ule mwangaza wa kweli, unaomwangazia kila mutu, unakuja katika dunia. Neno alikuwa yuko katika dunia, nayo dunia iliumbwa kwa njia yake, lakini ijapokuwa vile haikumutambua. Alikuja katika inchi yake, lakini taifa lake halikumupokea. Lakini wamoja waliomupokea, ndio wale waliomwamini, aliwapa uwezo wa kuwa watoto wa Mungu. Hawakuzaliwa kuwa watoto wa Mungu kwa namna ya kimutu, wala kwa mapenzi ya kimwili, wala kwa mapenzi ya mutu, lakini wamezaliwa na Mungu. Neno alifanywa kuwa mutu, naye akaishi kati yetu, akijaa neema na ukweli. Tuliona utukufu wake, utukufu ule Mwana wa pekee aliopewa na Baba. Yoane alimushuhudia akisema kwa sauti: “Huyu ndiye niliyesema juu yake: ‘Anayekuja nyuma yangu ananipita, kwa sababu alikuwa mbele sijazaliwa.’ ” Sisi wote tumepokea sehemu ya neema aliyojaa nayo, akitupatia baraka nyingi sana. Sheria ya Mungu ilitolewa kwa njia ya Musa, lakini neema na ukweli vilikuja kwa njia ya Yesu Kristo. Hakuna mutu aliyemwona Mungu wakati wowote. Lakini Mwana wa pekee anayekuwa Mungu, anayeishi pamoja na Baba, huyu ndiye aliyemutambulisha kwetu. Huu ndio ushuhuda wa Yoane kwa makuhani na Walawi waliotumwa na Wayuda kutoka Yerusalema kumwuliza kwamba yeye ni nani. Yoane aliwajibu hivi waziwazi bila kukana: “Mimi si Kristo.” Halafu wakamwuliza: “Basi wewe ni nani? Wewe ni Elia?” Yoane akajibu: “Mimi si yeye.” Wakamwuliza tena: “Wewe ni yule nabii?” Naye akawajibu: “Hapana.” Basi wakamwambia: “Wewe ni nani? Utuambie kusudi tuende kuwaelezea wale waliotutuma. Unasema nini juu yako mwenyewe?” Yoane akajibu: “Mimi ni sauti inayotangaza katika jangwa: ‘Munyooshe njia ya Bwana,’ ” sawa vile nabii Isaya alivyosema. Nao wale waliotumwa walikuwa Wafarisayo. Wakamwuliza Yoane: “Ikiwa wewe si Kristo, wala Elia, wala yule nabii, basi sababu gani unabatiza?” Yoane akawajibu: “Mimi ninabatiza kwa maji, lakini kati yenu kuna mutu ninyi musiyemujua, anayekuja nyuma yangu. Mimi sistahili hata kufungua kamba za viatu vyake.” Mambo hayo yalifanyika Betania, ngambo ya muto Yordani, pahali Yoane alipokuwa akibatiza. Kesho yake Yoane akamwona Yesu akikuja kwake, akasema: “Angalia Mwana-Kondoo wa Mungu anayeondoa zambi ya dunia! Huyu ndiye niliyesema juu yake kwamba mutu mumoja anakuja nyuma yangu, lakini ananipita kwa sababu alikuwa mbele sijazaliwa. Mimi sikumujua, lakini nimekuja kubatiza kwa maji kusudi ajulikane kwa taifa la Waisraeli.” Yoane akatoa ushuhuda huu: “Nimemwona Roho akishuka juu yake toka mbinguni kwa mufano wa njiwa na kukaa juu yake. Mimi sikumujua ni nani, lakini yule aliyenituma kubatiza kwa maji aliniambia: ‘Yule utakayemwona Roho akishuka juu yake na kukaa juu yake, mutu yule ndiye anayebatiza kwa Roho Mutakatifu.’ Mimi nimeona mambo haya, nami ninashuhudia kwamba huyu ndiye Mwana wa Mungu.” Kesho yake Yoane alikuwa pale tena pamoja na wawili kati ya wanafunzi wake. Wakati alipomwona Yesu akipita, akasema: “Angalia Mwana-Kondoo wa Mungu.” Wale wanafunzi wawili waliposikia maneno yale, wakamufuata Yesu. Yesu akageuka, akawaona wakimufuata, akawauliza: “Munatafuta nini?” Wakajibu: “Rabi (maana yake ‘Mwalimu’), unakaa wapi?” Naye akawajibu: “Mukuje na mutaona.” Basi wakaenda, wakaona pahali alipokaa, wakabaki pamoja naye siku ile. (Ilikuwa karibu na saa kumi ya magaribi.) Andrea, ndugu ya Simoni Petro, alikuwa mumoja wa wale wawili waliosikia maneno ya Yoane na kumufuata Yesu. Andrea alimukuta kwanza Simoni, ndugu yake wa tumbo na kumwambia: “Tumemwona Masiya” (maana yake “Kristo”). Kisha akamupeleka Simoni kwa Yesu. Yesu akamwangalia, akasema: “Wewe ndiwe Simoni mwana wa Yoane, sasa utaitwa Kefa.” (Jina “Kefa” ni sawasawa na “Petro” na maana yake ni “Jiwe.”) Siku iliyofuata Yesu alitaka kwenda Galilaya. Alipomukuta Filipo akamwambia: “Unifuate.” (Filipo alikuwa muzaliwa wa Betesaida, muji wa Andrea na Petro.) Kisha Filipo akamukuta Natanaeli, akamwambia: “Tumemwona yule ambaye Musa aliandika habari zake katika kitabu cha Sheria na ambaye manabii walisema juu yake. Ni Yesu wa Nazareti, mwana wa Yosefu.” Natanaeli akamwuliza: “Kuna kitu kizuri kinachoweza kutoka Nazareti?” Filipo akamujibu: “Kuja uone.” Wakati Yesu alipomwona Natanaeli akikuja kwake akasema hivi juu yake: “Angalia Mwisraeli wa kweli asiyekuwa na udanganyifu ndani yake hata kidogo!” Natanaeli akamwuliza: “Unanijua namna gani?” Yesu akamujibu: “Filipo alipokuwa hajakuita, nilikuona wakati ulipokuwa chini ya muti wa matunda ya tini.” Natanaeli akamwambia tena: “Mwalimu, wewe ni Mwana wa Mungu, wewe ni Mufalme wa Waisraeli.” Yesu akamujibu: “Unaamini kwa sababu nimekuambia kama nilikuona chini ya muti wa tini? Utaona mambo makubwa kuliko haya.” Yesu akaongeza kumwambia: “Kweli, kweli, ninawaambia: mutaona mbingu zimefunguka na wamalaika wa Mungu wakipanda na kushuka mpaka kwenye Mwana wa Mutu!” Siku mbili zilipopita, kulikuwa ndoa katika muji wa Kana, katika Galilaya. Mama ya Yesu alikuwa pale. Yesu alialikwa vilevile kwenye ndoa ile pamoja na wanafunzi wake. Wakati divai ilipomalizika, mama ya Yesu akamwambia: “Hawana divai tena.” Lakini Yesu akamujibu: “Mama, kuna maneno gani kati yako nami? Saa yangu haijatimia bado.” Halafu mama yake akawaambia watumishi: “Mufanye kila kitu atakachowaambia.” Pale kulikuwa mitungi sita iliyotengenezwa kwa mawe iliyotumiwa na Wayuda kwa kutilia maji ya kujitakasa. Ndani ya kila mumoja kuliweza kuingia yapata litre mia moja za maji. Yesu akawaambia watumishi: “Mujaze mitungi hii na maji.” Nao wakaijaza kabisa. Kisha Yesu akamwambia: “Muteke sasa kwa maji haya na muyapeleke kwa mukubwa wa karamu.” Watumishi wakayapeleka kwa mukubwa wa karamu, akaonja yale maji yaliyogeuka kuwa divai. Mukubwa ule hakujua pahali divai ile ilipotoka, lakini watumishi walioleta maji walijua. Basi akamwita bwana-arusi, na kumwambia: “Watu wote wanapatia waalikwa divai nzuri zaidi kwanza, kisha wakati wanapokwisha kunywa sana, wanawapatia ile isiyokuwa nzuri zaidi. Lakini wewe umechunga divai nzuri mpaka sasa.” Ni vile Yesu alivyofanya kitambulisho chake cha kwanza katika Kana ya Galilaya. Pale alionyesha utukufu wake na wanafunzi wake wakamwamini. Nyuma ya maneno yale, akaenda Kapernaumu pamoja na mama yake, wandugu zake na wanafunzi wake. Nao wakakaa kule siku chache. Wakati sikukuu ya Pasaka ya Wayuda ilipokaribia, Yesu akaenda Yerusalema. Akakuta watu katika hekalu wakiuzisha ngombe, kondoo na njiwa, na wengine wenye kubadilisha feza wakiikaa kwenye meza zao. Basi akasokota kamba kuwa fimbo na kuwafukuza wote toka hekalu pamoja na kondoo na ngombe wao. Kisha akapindua meza za wenye kubadilisha feza na kuzimwanga chini. Akawaambia wachuuzi wa njiwa: “Muondoshe vile vitu hapa. Musifanye nyumba ya Baba yangu kuwa nyumba ya biashara!” Wanafunzi wake wakakumbuka maneno haya yaliyoandikwa katika Maandiko Matakatifu: “Upendo wangu kwa ajili ya nyumba yako unanichoma.” Basi Wayuda wakamwuliza: “Utaonyesha kitambulisho gani kwa kutuhakikishia kwamba uko na haki ya kufanya hivi?” Yesu akawajibu: “Mubomoe hekalu hili, nami nitalijenga katika siku tatu.” Wayuda wakamwambia: “Hekalu hili lilijengwa kwa muda wa miaka makumi ine na sita, nawe utalijenga tena katika siku tatu?” Lakini hekalu ambalo Yesu alisema juu yake lilikuwa mwili wake. Wakati Yesu alipokwisha kufufuka, wanafunzi wake wakakumbuka kwamba alikuwa anasema juu ya jambo lile, wakaamini Maandiko Matakatifu na maneno yale aliyosema. Wakati ule Yesu alipokuwa Yerusalema kwa sikukuu ya Pasaka, watu wengi walimwamini kwa sababu waliona vitambulisho alivyofanya. Lakini Yesu hakuwaaminia kwa sababu aliwajua wote vizuri. Naye hakuhitaji kupewa ushuhuda juu ya mutu yeyote, kwa maana yeye mwenyewe alijua yanayokuwa ndani ya mioyo ya watu. Kulikuwa mutu mumoja aliyeitwa Nikodemo, mukubwa wa Wayuda, aliyekuwa mumoja wa kundi la Wafarisayo. Alimwendea Yesu usiku na kumwambia: “Mwalimu, tunajua kama Mungu amekutuma kufundisha, kwa maana hakuna mutu anayeweza kuonyesha vitambulisho hivi unavyoonyesha isipokuwa anaongozwa na Mungu.” Yesu akamujibu: “Kweli, kweli ninakuambia: mutu hawezi kuingia katika Ufalme wa Mungu asipozaliwa mara ya pili.” Nikodemo akamwuliza: “Namna gani mutu anaweza kuzaliwa akiwa muzee? Anaweza kurudi ndani ya tumbo la mama yake na kuzaliwa mara ya pili?” Yesu akajibu: “Kweli, kweli ninakuambia: mutu asipozaliwa kwa maji na kwa Roho, hawezi kuingia katika Ufalme wa Mungu. Kinachozaliwa na mutu ni cha kimwili, nacho kinachozaliwa na Roho ni cha kiroho. Usishangae kwa sababu nimekuambia kwamba sherti ninyi muzaliwe mara ya pili. Upepo unavuma pahali unapotaka, nawe unasikia sauti yake, lakini haujui pahali unapotoka wala unapokwenda. Na ni vile inavyokuwa kwa kila mutu anayezaliwa kwa Roho.” Basi Nikodemo akamwuliza: “Maneno haya yanawezekana namna gani?” Yesu akamujibu: “Wewe unayekuwa mwalimu mukubwa katika inchi ya Israeli, haujui maneno haya? Kweli, kweli ninakuambia: tunasema maneno tunayojua na kushuhudia maneno tuliyoona, lakini ninyi hamutaki kupokea ushuhuda wetu. Ikiwa hamwamini wakati ninapowaambia maneno ya dunia, namna gani mutaamini kama nikiwaambia maneno ya mbinguni? Na zaidi ya hii hakuna mutu aliyepanda mbinguni, isipokuwa Mwana wa Mutu aliyeshuka toka mbinguni. Sawa Musa alivyonyanyua nyoka ya shaba juu ya muti katika jangwa, ni hivi vilevile, sherti Mwana wa Mutu anyanyuliwe, kusudi kila mutu anayemwamini apate uzima wa milele. Kwa maana Mungu alipenda sana ulimwengu hata kumutoa Mwana wake wa pekee, kusudi kila mutu anayemwamini asipotee, lakini apate uzima wa milele. Mungu hakumutuma Mwana wake katika ulimwengu kusudi ahukumu ulimwengu, lakini kusudi ulimwengu uokolewe naye. Anayemwamini Mwana hahukumiwi, lakini asiyemwamini amekwisha kuhukumiwa, kwa sababu hakumwamini Mwana wa pekee wa Mungu. Hukumu inatokana na hivi: mwangaza umekuja katika ulimwengu, lakini watu wanapenda giza kuliko mwangaza, kwa sababu matendo yao ni mabaya. Kila mutu anayefanya mabaya anachukia mwangaza, naye anakataa kuja kwenye mwangaza, kusudi matendo yake yasionekane wazi. Lakini anayeshika ukweli, anakuja kwenye mwangaza, kusudi matendo yake yaonekane wazi kwamba yanatendeka sawa Mungu anavyoamuru.” Kisha mambo hayo, Yesu na wanafunzi wake wakaenda Yudea. Akabaki kule pamoja nao na kubatiza. Yoane vilevile alikuwa akibatiza kule Ainoni, karibu na Salimu, kwa sababu kule kulikuwa maji mengi. Watu walimwendea, naye akawabatiza. (Wakati ule Yoane alikuwa hajawekwa katika kifungo.) Kulitokea mabishano kati ya wanafunzi wa Yoane na Muyuda mumoja juu ya desturi zao za kujitakasa. Basi wakamwendea Yoane na kumwambia: “Mwalimu, unakumbuka yule mutu aliyekuwa pamoja nawe ngambo ya Yordani, yule uliyemushuhudia? Angalia sasa, yeye anabatiza, na watu wote wanamufikia!” Yoane akawajibu: “Hakuna mutu anayeweza kuwa na kitu isipokuwa amekipewa na Mungu. Ninyi wenyewe ni washuhuda wangu kwamba nilisema: ‘Mimi si Kristo, lakini nimetumwa mbele yake.’ Mwenye bibi arusi ndiye bwana-arusi; lakini rafiki ya bwana arusi anasimama karibu naye na kumusikiliza, anafurahi sana kusikia sauti ya bwana-arusi. Na ni hivi mimi ninafurahi, na furaha yangu imetimia sasa. Sherti utukufu wake uzidi na wangu upunguke. “Anayetoka juu ni juu ya yote; anayekuwa wa dunia ni wa dunia, naye anasema maneno ya dunia. Anayetoka mbinguni ni juu ya yote; anashuhudia yale aliyoyaona na kuyasikia, lakini hakuna mutu anayekubali ushuhuda wake. Yeyote anayekubali ushuhuda wake anahakikisha kama Mungu ni mwenye ukweli. Aliyetumwa na Mungu anasema maneno ya Mungu, kwa sababu Mungu anamujaza Roho wake kwa uwingi. Baba anamupenda Mwana wake, naye ameweka vitu vyote kwa mukono wake. Anayemwamini Mwana yuko na uzima wa milele. Anayekataa kumwamini Mwana hatapata uzima; atakaa akipatwa na kasirani ya Mungu.” Yesu akatambua kwamba Wafarisayo wamepata habari kama yeye anapata wanafunzi wengi zaidi kuliko Yoane na kuwabatiza. (Hakika Yesu mwenyewe hakubatiza mutu lakini ni wanafunzi wake.) Basi, Yesu akaondoka Yudea na kurudi Galilaya. Kwa kufika kule ilimupasa apite katika Samaria. Akafika karibu na muji mumoja wa Samaria unaoitwa Sikari, uliokuwa karibu na shamba lile Yakobo alilomupa mwana wake Yosefu. Pale kulikuwa kisima kilichokuwa cha Yakobo. Yesu akaikaa kwa ukingo wa kisima, kwa sababu alikuwa amechoka na safari. Ilikuwa karibu na saa sita za muchana. Halafu mwanamuke mumoja Musamaria akakuja kuteka maji. Na Yesu akamwambia: “Unipe maji ya kunywa.” (Wakati ule wanafunzi wake walikuwa wamekwenda katika muji kununua vyakula.) Basi yule mwanamuke Musamaria akamwambia Yesu: “Namna gani wewe Muyuda unaweza kuniomba mimi Musamaria maji ya kunywa?” (Wayuda hawakukuwa na ushirika na Wasamaria.) Yesu akamujibu: “Kama ungejua kitu Mungu anachoweza kukupatia, na ni nani anayekuomba maji ya kunywa, wewe ndiwe ungemwomba, naye angekupa maji ya uzima.” Yule mwanamuke akamwambia: “Bwana, hauna chombo cha kutekea, na kisima ni kirefu sana. Basi umepata wapi maji ya uzima? Babu yetu Yakobo ndiye aliyetupa sisi kisima hiki, hata yeye mwenyewe pamoja na wana wake na nyama wake walikunywa maji yake. Wewe unajiona kuwa mukubwa kuliko Yakobo?” Yesu akamujibu: “Kila mutu anayekunywa maji haya atasikia kiu tena; lakini yeyote atakayekunywa maji yale nitakayomupa, hatasikia kiu tena hata kidogo. Maji nitakayomupa yatakuwa ndani yake kama chemichemi inayotiririka maji ya uzima wa milele.” Mwanamuke yule akamwambia: “Bwana, unipe basi maji yale, kusudi nisisikie kiu tena. Hivi sitahitaji kuja tena hapa kuteka maji.” Yesu akamwambia: “Uende kumwita mume wako na urudi naye hapa.” Yule mwanamuke akamujibu: “Sina mume.” Na Yesu akamwambia: “Unasema kweli kwamba hauna mume; kwa maana ulikuwa na wanaume watano, na yule unayeishi naye sasa si mume wako. Hivi unasema ukweli.” Halafu mwanamuke yule akamwambia: “Bwana, ninaona kama wewe ni nabii. Babu zetu walimwabudu Mungu juu ya mulima huu, lakini ninyi Wayuda munasema kama Yerusalema ni pahali pa kumwabudia Mungu.” Yesu akamwambia: “Ee mama, unisadiki; kutakuwa wakati hamutamwabudu Baba juu ya mulima huu wala Yerusalema. Ninyi Wasamaria hamujui munachokiabudu; sisi tunajua tunachokiabudu kwa sababu wokovu unatokea kwa njia ya Wayuda. Lakini kutakuwa wakati, nao umekwisha kutimia, wale wanaoabudu kwa kweli watakapomwabudu Baba katika roho na ukweli; kwa maana Baba anataka watu wanaoabudu kwa namna ile. Mungu ni roho, nao wanaomwabudu wanapaswa kumwabudu katika roho na ukweli.” Mwanamuke yule akamwambia: “Ninajua kwamba Masiya anayeitwa Kristo, atakuja. Na wakati atakapokuja atatuelezea maneno yote.” Yesu akamujibu: “Mimi ninayesema nawe, ndiye.” Saa ile ile wanafunzi wa Yesu wakarudi, nao wakashangaa kumwona akisemezana na mwanamuke. Lakini hakuna mumoja wao aliyemwuliza yule mwanamuke kwamba anataka nini au kumwuliza Yesu kwamba sababu gani anasema naye. Basi mwanamuke yule akaacha mutungi wake wa maji pale, akarudi katika muji na kuwaambia watu: “Mukuje mumwone mutu aliyeniambia maneno yote niliyotenda. Huyu si Kristo?” Basi wakatoka katika muji na kumwendea Yesu. Wakati ule wanafunzi wa Yesu walimusihi, wakisema: “Mwalimu, kula chakula.” Lakini akawajibu: “Mimi nina chakula musichokijua.” Basi wanafunzi wakaanza kuulizana: “Kuna mutu aliyemuletea chakula?” Yesu akawaambia: “Chakula changu ni kufanya mapenzi ya yule aliyenituma na kutimiza kazi yake. Si ninyi munazoea kusema: ‘Kunabaki miezi mine kuwe mavuno’? Lakini mimi ninawaambia, muinue macho, muangalie mashamba; mimea imekomaa, nayo ni tayari kwa kuvunwa. Muvunaji anakwisha kupokea mushahara, naye anakusanya mavuno kwa ajili ya uzima wa milele, kusudi mupandaji na muvunaji wafurahi pamoja. Kwa maana neno hili ni kweli: ‘Mutu mumoja anapanda na mwingine anavuna.’ Mimi niliwatuma ninyi katika shamba kuvuna mavuno ambayo hamukusumbukia; wengine waliyasumbukia, nanyi mumepata faida ya kazi yao.” Wasamaria wengi wa muji ule walimwamini Yesu kwa sababu ya maneno ya yule mwanamuke aliposhuhudia hivi: “Aliniambia mambo yote niliyotenda.” Na Wasamaria walipomufikia Yesu, walimusihi akae pamoja nao, naye akakaa kule muda wa siku mbili. Wengine wengi zaidi waliamini kwa sababu ya maneno yake mwenyewe, nao wakamwambia yule mwanamuke: “Sasa tunaamini, si kwa sababu ya maneno uliyotuambia tu, lakini kwa sababu tumesikia sisi wenyewe na tunajua hakika kwamba huyu ni Mwokozi wa dunia.” Siku mbili zilipopita, Yesu akaondoka kule, akaenda Galilaya. Yesu mwenyewe alikuwa ameshuhudia kwamba nabii haheshimiwi katika inchi yake mwenyewe, lakini alipofika Galilaya, wakaaji wa kule wakamupokea, kwa maana wao vilevile walikuwa Yerusalema kwa sikukuu ya Pasaka, nao waliona mambo yote aliyofanya kule. Basi Yesu akarudi tena Galilaya katika muji Kana, pahali alipogeuza maji kuwa divai. Kule kulikuwa mukubwa mumoja wa serikali, aliyekuwa na mwana mugonjwa katika muji Kapernaumu. Wakati aliposikia kwamba Yesu amefika Galilaya toka Yudea, mukubwa huyu akamwendea, akamusihi aende Kapernaumu kumuponyesha mwana wake, aliyekuwa karibu kufa. Basi Yesu akamwambia: “Ninyi hamuwezi kuamini hata kidogo kama musipoona vitambulisho na maajabu.” Yule mukubwa wa serikali akamujibu: “Bwana, ninakuomba ufike kwangu mbele mutoto wangu hajakufa.” Yesu akamwambia: “Kwenda tu, mwana wako ni muzima.” Mutu yule akaamini neno Yesu alilosema, naye akaondoka. Alipokuwa katika njia akirudi kwake, watumishi wake wakakuja kukutana naye na kumwambia kwamba mutoto wake ni muzima. Halafu akawauliza saa gani mutoto alipoanza kujisikia vizuri. Nao wakamujibu: “Yeye alipona homa jana muchana saa saba.” Basi baba yule akatambua kama ilikuwa ni saa ile ile Yesu alipomwambia kwamba mwana wake ni muzima. Basi yeye na jamaa yake yote wakamwamini Yesu. Hiki ndicho kitambulisho cha pili Yesu alichoonyesha. Ilikuwa wakati aliporudi Galilaya akitoka Yudea. Nyuma ya maneno hayo, Yesu akaenda Yerusalema kwa sikukuu ya Wayuda. Kule Yerusalema, karibu na mulango wa muji huu unaoitwa “Mulango wa Kondoo,” kuna kisima chenye viingilio vitano vyenye paa. Kisima kile kinaitwa katika Kiebrania “Betesaida.” Wagonjwa wengi walikuwa wakilala katika viingilio vile; kulikuwa vipofu, vilema na wenye kupooza. [Walikuwa wakingoja maji yatikiswe, kwa sababu malaika wa Bwana alishuka mara kwa mara ndani ya kile kisima na kutikisa maji. Na mugonjwa wa kwanza aliyeingia ndani ya maji kisha kuyatikisa, alipona ugonjwa wowote aliokuwa nao.] Pale kulikuwa mutu mumoja aliyekuwa mugonjwa tangia miaka makumi tatu na minane. Wakati Yesu alipomwona akilala na kutambua kwamba amekuwa mugonjwa kwa muda wa siku nyingi, akamwuliza: “Unataka kupona?” Yule mugonjwa akamujibu: “Bwana, sina mutu wa kuniingiza katika kisima wakati maji yanapotikiswa, nami ninapojaribu kuingia ndani ya maji, mutu mwingine anaingia mbele yangu.” Yesu akamwambia: “Simama, utwae kipoyi chako na uende.” Mara moja mutu yule akapona, akatwaa kipoyi chake na kuanza kutembea. Siku ile ilikuwa siku ya Sabato, kwa hiyo Wayuda wakamwambia mutu yule aliyeponyeshwa: “Leo ni siku ya Sabato, na Sheria haikuruhusu kubeba kipoyi chako.” Akawajibu: “Yule aliyeniponyesha ndiye aliyeniambia: ‘Twaa kipoyi chako na uende.’ ” Basi wakamwuliza kwamba ni nani aliyemwambia kwamba atwae kipoyi wake na aende. Lakini mutu yule aliyeponyeshwa hakujua ni nani, kwa maana Yesu alikuwa amekwisha kuondoka katikati ya kundi kubwa la watu waliokuwa pale. Kisha Yesu akamukuta mutu yule ndani ya hekalu, akamwambia: “Angalia, sasa umepona. Basi usifanye zambi tena, kusudi jambo baya zaidi lisikufikie.” Yule mutu akaenda kuwaambia Wayuda kwamba Yesu ndiye aliyemuponyesha. Kwa sababu ile Wayuda wakaanza kumufuatilia Yesu kwa kuwa alifanya mambo haya kwa siku ya Sabato. Lakini Yesu akawajibu: “Baba yangu anatumika wakati wote, nami ninatumika vilevile.” Kwa ajili ya neno hili Wayuda walitaka tena zaidi kumwua; si kwa sababu ya kuvunja Sheria ya siku ya Sabato tu, lakini vilevile kwa sababu alisema kwamba Mungu ni Baba yake, akijifanya hivi kuwa sawasawa na Mungu. Basi Yesu akaongeza kuwaambia Wayuda: “Kweli, kweli, ninawaambia: Mwana hawezi kufanya kitu kwa mafikiri yake mwenyewe; anafanya tu kile ambacho anaona Baba akifanya. Na mambo yote Baba anayofanya, Mwana anayafanya vilevile. Kwa maana Baba anamupenda Mwana, anamwonyesha yote anayofanya yeye mwenyewe. Atamwonyesha mambo makubwa zaidi kuliko haya kusudi mupate kushangaa. Kwa maana kama vile Baba anavyofufua wafu na kuwarudishia uzima, vile vile Mwana anawapa uzima wale anaowataka. Na zaidi ya hii Baba hahukumu hata mutu mumoja, lakini amemupa Mwana uwezo wote wa kuhukumu, kusudi watu wote wamuheshimu Mwana kama vile wanavyomuheshimu Baba. Asiyemuheshimu Mwana, hamuheshimu Baba aliyemutuma. “Kweli, kweli ninawaambia: anayesikia neno langu na kumwamini yule aliyenituma, anapata uzima wa milele. Yeye hatahukumiwa, lakini ameponyoka lufu na kupata uzima. Kweli, kweli ninawaambia: kutakuwa wakati, nao umekwisha kutimia, wafu watakaposikia sauti ya Mwana wa Mungu, na wale wanaoisikia, wataishi. Kama vile Baba ana uwezo wa kupana uzima, ndivyo vilevile amemupa Mwana uwezo wa kupana uzima. Vilevile amemupa Mwana mamlaka ya kuhukumu, kwa sababu yeye ni Mwana wa Mutu. Musishangae kwa ajili ya maneno haya, kwa sababu kutakuwa wakati wafu wote wanaokuwa ndani ya makaburi watakaposikia sauti yake na kutoka ndani ya makaburi yao. Waliotenda mema watafufuka na kupata uzima, lakini waliotenda mabaya watafufuka na kuhukumiwa. “Siwezi kufanya kitu kwa mafikiri yangu mwenyewe. Ninahukumu tu kama vile Mungu anavyoniambia na hukumu yangu ni ya haki, kwa sababu sitafuti kufanya mapenzi yangu, lakini mapenzi ya yule aliyenituma. Kama nikijishuhudia mimi mwenyewe, ushuhuda wangu hauwezi kukubaliwa kuwa wa kweli. Lakini kuna mwingine anayenishuhudia, nami ninajua kwamba ushuhuda anaoutoa juu yangu ni wa kweli. Ninyi mulituma wajumbe kwa Yoane, naye alishuhudia ukweli. Kweli mimi sihitaji kushuhudiwa na mutu, lakini ninasema maneno haya kusudi mupate kuokolewa. Yoane alikuwa kama taa inayowaka na kuangaza, na ninyi mulipendezwa kufurahishwa na mwangaza wake kwa muda. Lakini mimi nina ushuhuda mukubwa zaidi kuliko ule uliotolewa na Yoane. Maana sasa mambo ninayofanya ndiyo Baba aliyoniamuru kutimiza, nayo yananishuhudia na kuonyesha kwamba yeye amenituma. Na Baba aliyenituma amenishuhudia vilevile. Ninyi hamujasikia sauti yake wakati wowote wala hamujaona sura yake. Ninyi hamuchungi neno lake ndani yenu, kwa sababu ninyi hamumwamini yule aliyetumwa naye. Munachunguza Maandiko Matakatifu, kwa maana munazani kuwa ndani yao mutapata uzima wa milele. Maandiko hayo ndiyo yanayonishuhudia, lakini ninyi hamutaki kuja kwangu mupate uzima. “Mimi sipokei sifa kutoka kwa watu. Lakini ninawajua ninyi kwamba hamumupendi Mungu. Mimi nimekuja kwa jina la Baba yangu, nanyi hamutaki kunipokea. Lakini ikiwa mwingine anakuja kwa jina lake mwenyewe, ninyi mutamupokea. Basi namna gani mutaweza kuamini, ninyi munaopokea sifa kutoka wamoja kwa wengine, lakini hamutafuti sifa inayotoka kwake anayekuwa Mungu peke yake? Musizanie kwamba mimi nitawashitaki kwa Baba. Atakayewashitaki ninyi ni Musa, ambaye mulimutumainia. Kama mungemusadiki Musa, mungenisadiki mimi vilevile, kwa sababu yeye aliandika habari juu yangu. Lakini ikiwa hamusadiki yale Musa aliyoandika, namna gani mutasadiki maneno ninayosema?” Nyuma ya maneno hayo, Yesu akavuka ziwa la Galilaya (linaloitwa vilevile Tiberia). Kundi kubwa la watu wakamufuata, kwa sababu watu hao waliona vitambulisho alivyoonyesha kwa kuponyesha wagonjwa. Yesu akapanda kwenye kilima, na kuikaa kule pamoja na wanafunzi wake. Na Pasaka, ambayo ni moja ya sikukuu za Wayuda, ilikuwa karibu. Wakati Yesu alipoinua macho, akaona kundi kubwa la watu wakimufikia. Halafu akamwuliza Filipo: “Wapi tunaweza kununua vyakula kwa kulisha watu hawa?” (Alisema vile kusudi amupime Filipo, kwa sababu yeye mwenyewe alijua atakavyofanya.) Filipo akamujibu: “Hata tukinunua mikate kwa bei ya vikoroti mia mbili vya feza, haitatosha kwa kumupa kila mutu hata kidogo tu.” Mwanafunzi wake mwingine mumoja anayeitwa Andrea, ndugu ya Simoni Petro, akamwambia: “Hapa kuna mutoto mumoja anayekuwa na mikate mitano ya shayiri pamoja na samaki mbili. Lakini chakula hiki hakitawafalia kitu watu wengi kama hawa.” Yesu akasema: “Muwaambie watu waikae chini.” (Pale kulikuwa majani mengi.) Basi wakaikaa chini; na hesabu ya wanaume tu ilikuwa yapata elfu tano. Kisha Yesu akatwaa ile mikate, akamushukuru Mungu na kuigawanya kwa watu walioikaa pale. Akawapa samaki vilevile kwa kadiri walivyotaka. Walipokwisha kushiba, Yesu akawaambia wanafunzi wake: “Mukusanye vipande vinavyobaki, kusudi kusipotee kitu.” Basi wakavikusanya, wakajaza vitunga kumi na viwili na vipande vilivyobaki vya ile mikate mitano ya shayiri waliyokula. Watu walipoona kile kitambulisho Yesu alichoonyesha, wakasema: “Hakika mutu huyu ndiye yule nabii aliyepaswa kuja katika dunia!” Wakati Yesu alipotambua kama walitaka kuja kumutwaa kwa nguvu na kumuweka kuwa mufalme, akaondoka na kwenda tena kwa kilima peke yake. Ilipokuwa magaribi, wanafunzi wake wakashuka kwenda kwenye ziwa. Wakaingia ndani ya chombo, wakaanza kuvuka ziwa kwa kwenda Kapernaumu. Giza lilikuwa limekwisha kuwa, na Yesu alikuwa hajarudi kukutanana nao. Ziwa likaanza kuchafuka sana; kwa sababu upepo ulikuwa ukivuma kwa nguvu. Walipofika umbali wa kadiri ya kilometre tano au sita, wakamwona Yesu anakaribia chombo, akitembea juu ya maji; kwa hiyo wakaogopa. Lakini Yesu akawaambia: “Ni mimi, musiogope!” Wao walitaka kumupandisha ndani ya chombo lakini mara moja chombo kikafikia inchi kavu, pahali walipokuwa wakienda. Kesho yake watu waliobaki kule ngambo ya ziwa wakatambua kwamba kulikuwa tu chombo kimoja pale. Walijua vilevile kwamba Yesu hakuingia ndani ya chombo pamoja na wanafunzi wake, lakini wanafunzi wake walikwenda peke yao. Na vilevile vyombo vingine vilivyotoka katika muji Tiberia vilifika karibu na pahali pale walipokula mikate, Bwana alipokuwa amekwisha kushukuru Mungu. Wakati walipoona kama Yesu hakukuwa pale wala wanafunzi wake, wakajiingilia ndani ya vyombo vile na kwenda Kapernaumu kumutafuta Yesu. Watu wale wakamukuta Yesu kule ngambo ya ziwa na kumwuliza: “Mwalimu, ulifika hapa wakati gani?” Yesu akawajibu: “Kweli, kweli ninawaambia: hamunitafuti kwa sababu muliona vitambulisho nilivyoonyesha, lakini kwa sababu mulikula mikate na kushiba. Musitumikie chakula kinachoharibika, lakini mutumikie chakula kinachodumu na kuleta uzima wa milele. Mwana wa Mutu atawapa ninyi chakula hiki, kwa sababu Mungu Baba ametoa uhakikisho juu yake.” Basi wakamwuliza: “Tufanye nini kusudi tupate kutumika kazi ya Mungu?” Yesu akawajibu: “Hii ndiyo kazi ya Mungu: mumwamini yule aliyemutuma.” Wakamwuliza: “Basi utatuonyesha kitambulisho gani kusudi tupate kukiona na kukuamini? Utafanya jambo gani? Babu zetu walikula mana katika jangwa, kama ilivyoandikwa katika Maandiko Matakatifu yanayosema: ‘Aliwakulisha kwa mukate uliotoka mbinguni.’ ” Yesu akawajibu: “Kweli, kweli ninawaambia: Musa hakuwapa ninyi mukate wa mbinguni, lakini ni Baba yangu anayewapa ninyi mukate wa kweli wa mbinguni. Maana mukate Mungu anaoupana ni yule anayeshuka toka mbinguni na kuleta uzima katika dunia.” Basi wakamwambia: “Bwana, utupatie mukate ule siku zote.” Yesu akawaambia: “Mimi ni mukate wa uzima. Anayenikubali hatasikia njaa hata kidogo, na yule anayeniamini hatasikia kiu hata kidogo. Lakini kama nilivyowaambia: mumeniona, lakini ijapokuwa vile hamuamini. Wote Baba anaonipa wanakuja kwangu; nami sitamukataa hata kidogo yule anayekuja kwangu. Kwa sababu nimeshuka toka mbinguni kusudi nifanye mapenzi ya yule aliyenituma, wala si mapenzi yangu. Na mapenzi ya yule aliyenituma ni kwamba nisipoteze hata mumoja wa wale alionipa, lakini nimufufue siku ya mwisho wa dunia. Hakika mapenzi ya Baba yangu ni kwamba kila mutu anayemwona Mwana na kumwamini apate uzima wa milele, nami nitamufufua siku ya mwisho.” Basi Wayuda wakaanza kunungunika kwa sababu Yesu alisema kwamba yeye ni mukate ulioshuka toka mbinguni. Nao wakasema: “Huyu si Yesu mwana wa Yosefu? Si tunawajua baba yake na mama yake? Namna gani anaweza kusema sasa kwamba alishuka toka mbinguni?” Yesu akawajibu: “Musikuwe na manunguniko kati yenu. Hakuna mutu anayeweza kuja kwangu, isipokuwa anavutwa na Baba aliyenituma, nami nitamufufua siku ya mwisho. Imeandikwa hivi katika maandiko ya manabii: ‘Wote watafundishwa na Mungu.’ Kila mutu anayemusikia Baba na kufuata mafundisho yake, anakuja kwangu. Si kusema kwamba kuna mutu yeyote aliyemwona Baba isipokuwa yule aliyetoka kwa Mungu; yeye ndiye aliyemwona Baba. Kweli, kweli ninawaambia: anayeamini anapata uzima wa milele. Mimi ni mukate wa uzima. Babu zenu walikula mana katika jangwa, lakini wakakufa. Lakini ule ni mukate ulioshuka toka mbinguni, anayeukula hatakufa. Mimi ni ule mukate wa uzima, ulioshuka toka mbinguni. Kama mutu akikula mukate huu ataishi milele. Na mukate nitakaotoa ni mwili wangu, utakaotolewa kusudi dunia ipate uzima.” Basi Wayuda wakaanza kubishana sana kati yao, wakasema: “Namna gani mutu huyu anaweza kutupatia mwili wake tuukule?” Kwa hiyo Yesu akawaambia: “Kweli, kweli, ninawaambia: musipokula mwili wa Mwana wa Mutu na kunywa damu yake, hamutakuwa na uzima ndani yenu. Anayekula mwili wangu na kunywa damu yangu anapata uzima wa milele, nami nitamufufua siku ya mwisho. Mwili wangu ni chakula cha kweli na damu yangu ni kinywaji cha kweli. Anayekula mwili wangu na kunywa damu yangu anakaa ndani yangu, nami ninakaa ndani yake. Kama vile Baba aliyenituma anavyokuwa muzima, nami ninaishi kwa nguvu zake, vilevile anayenikula ataishi kwa nguvu zangu. Huu ndio mukate ulioshuka toka mbinguni, nao si kama mukate ule babu zenu waliokula katika jangwa na kufa. Anayekula mukate huu ataishi milele.” Yesu alisema maneno haya wakati alipokuwa akifundisha katika nyumba ya kuabudia kule Kapernaumu. Wengi kati ya wanafunzi wake waliposikia maneno haya, wakasema: “Masemi haya ni magumu. Ni nani anayeweza kuyakubali?” Yesu akafahamu kwamba wanafunzi wake wananungunika juu ya neno hili; basi akawauliza: “Neno hili linawakwaza? Basi itakuwa namna gani kama mukimwona Mwana wa Mutu akipanda tena pahali alipokuwa mbele? Roho ndiye anayeleta uzima; mwili hauwezi kufaa kitu. Maneno haya niliyosema nanyi, ndiyo Roho na uzima. Lakini kuna wengine kati yenu wasioamini.” (Yesu alisema vile kwa sababu alijua tangu mwanzo wale wasioamini na yule atakayemutoa.) Yesu akaongeza kusema: “Kwa sababu hii niliwaambia kama hakuna mutu anayeweza kuja kwangu, isipokuwa anawezeshwa na Baba.” Basi kwa sababu ya maneno haya, wengi kati ya wanafunzi wake wakamwacha, nao hawakutembea tena pamoja naye. Kwa hiyo Yesu akawauliza wale wanafunzi kumi na wawili: “Nanyi munataka kwenda vilevile?” Simoni Petro akamujibu: “Bwana, tutakwenda kwa nani? Wewe unasema maneno ya uzima wa milele. Na sasa tunaamini na kujua kwamba wewe ni Mutakatifu wa Mungu.” Yesu akawajibu: “Ni mimi peke niliyewachagua ninyi kumi na wawili, lakini ingawa hivi mumoja wenu ni Shetani!” (Alisema hivi juu ya Yuda mwana wa Simoni Iskariota, kwa maana yeye ndiye atakayemutoa, ijapokuwa alikuwa mumoja wa wale kumi na wawili.) Kisha mambo hayo, Yesu akatembea katika Galilaya. Hakutaka kutembea katika Yudea, kwa sababu Wayuda walitaka kumwua. Sikukuu moja ya Wayuda inayoitwa Sikukuu ya Vibanda ilipokuwa karibu, wandugu za Yesu wakamwambia: “Ondoka hapa, uende Yudea kusudi wanafunzi wako waone matendo unayofanya. Hakuna mutu anayefanya kitu kwa uficho, ikiwa anataka kujulikana waziwazi. Basi kwa kuwa unafanya matendo kama hayo, ujionyeshe mbele ya watu wote.” (Hata wandugu zake vilevile hawakumwamini.) Na Yesu akawaambia: “Wakati unaofaa kwangu haujatimia; lakini wakati wowote unafaa kwenu. Watu wa dunia hawawezi kuwachukia ninyi, lakini wananichukia mimi kwa sababu ninashuhudia kwamba matendo yao ni mabaya. Ninyi muende kwa sikukuu. Mimi sijaenda bado kwa sikukuu hii, kwa sababu wakati unaofaa kwangu haujatimia.” Alipokwisha kuwaambia maneno hayo, akabaki Galilaya. Wandugu zake walipokwisha kwenda kwa sikukuu ile, Yesu akaenda kule vilevile, lakini alienda kwa siri bila kujionyesha waziwazi. Wayuda walikuwa wakimutafuta kwenye sikukuu ile na kuuliza kwamba yeye yuko wapi. Katika kundi lile kulikuwa manunguniko mengi juu yake. Wamoja walisema: “Yeye ni mutu muzuri.” Wengine walisema: “Hapana, si vile, yeye anawadanganya watu.” Lakini hakuna mutu aliyesema juu yake waziwazi, kwa sababu waliwaogopa wakubwa wa Wayuda. Halafu katikati ya sikukuu, Yesu akaingia ndani ya hekalu na kuanza kufundisha. Wayuda wakashangaa, wakisema: “Mutu huyu amepata elimu kama hii namna gani, naye hakufundishwa?” Yesu akawajibu: “Mafundisho ninayotoa si yangu, lakini ni ya yule aliyenituma. Kama mutu akitaka kufanya mapenzi ya Mungu, atajua kama mafundisho yangu yanatoka kwa Mungu, au kama ninasema kwa mamlaka yangu mwenyewe. Mutu anayesema kwa mamlaka yake mwenyewe, anajitafutia sifa yake mwenyewe. Lakini yeye anayetafuta sifa ya yule aliyemutuma, huyu ni mwenye ukweli wala hana ubaya wowote. Musa hakuwapa ninyi Sheria? Ingawa hivyo hakuna mumoja wenu anayetii Sheria. Na sasa sababu gani munatafuta kuniua?” Watu wale wakajibu: “Wewe uko na pepo. Nani anatafuta kukuua?” Yesu akawajibu: “Nilifanya jambo moja, nalo limewashangaza ninyi wote. Ninyi munatahiri watu hata kwa siku ya Sabato kwa sababu Musa aliwatolea ninyi amri ya kutahiri, (kwa hakika haikutoka kwa Musa, lakini kwa babu zenu). Basi, kama munaweza kutahiri mutu kwa siku ya Sabato, kusudi musivunje Sheria ya Musa, kwa nini munanikasirikia kwa sababu nimemuponyesha mutu kabisa kwa siku ya Sabato? Muache kuhukumu kufuatana na hali ya inje, lakini muhukumu kwa haki.” Halafu watu wamoja wa Yerusalema wakasema: “Huyu si mutu yule wanayetafuta kumwua? Angalia, anasema waziwazi wala hawamwambii neno! Labda wakubwa nao wametambua kweli kuwa huyu ndiye Kristo. Lakini tunajua pahali mutu huyu anapotoka. Kristo atakapokuja, hakuna mutu atakayejua pahali atakapotokea.” Basi Yesu alipokuwa akifundisha katika hekalu akasema hivi kwa sauti: “Ndiyo, ninyi munajidai kwamba munanijua na munajua pahali ninapotoka. Sikukuja kwa mamlaka yangu mwenyewe, lakini aliyenituma ni mwenye ukweli. Ninyi hamumujui, lakini mimi ninamujua sababu nilitoka kwake, naye ndiye aliyenituma.” Basi wakatafuta kumufunga, lakini hakuna mutu aliyemukamata, kwa sababu saa yake ilikuwa haijatimia. Watu wengi katika kundi lililokuwa pale wakamwamini, wakisema: “Kristo atakapokuja, ataonyesha vitambulisho zaidi kuliko mutu huyu?” Wafarisayo wakasikia maneno hayo watu waliyosemasema juu ya Yesu. Basi wakubwa wa makuhani na Wafarisayo wakatuma walinzi wao kumufunga. Yesu akasema: “Ningali pamoja nanyi kwa wakati kidogo na kisha nitarudi kwa yule aliyenituma. Mutanitafuta, lakini hamutaniona, kwa maana hamuwezi kufika pahali nitakapokuwa.” Wayuda wakaulizana hivi wao kwa wao: “Mutu huyu atakwenda wapi sisi tusipoweza kumwona? Ataenda kwa Wayuda waliosambazwa kati ya Wagriki na kuwafundisha Wagriki? Yeye anasema kwamba tutamutafuta, lakini hatutamwona, na kwamba hatuwezi kufika pahali atakapokwenda. Maana ya maneno haya ni gani?” Siku ya mwisho ya sikukuu ile iliyokuwa siku kubwa, Yesu akasimama na kusema hivi kwa sauti: “Mutu akiwa na kiu, akuje kwangu akunywe. Kama vile Maandiko Matakatifu yanavyosema: ‘Mito ya maji ya uzima yatatiririka toka ndani ya yule anayeniamini.’ ” (Alisema vile juu ya Roho atakayepokelewa na wale wanaomwamini Yesu. Kwa wakati ule Roho alikuwa hajatumwa bado, kwa sababu Yesu alikuwa hajatukuzwa.) Watu wamoja katika kundi lile waliposikia maneno hayo, wakasema: “Hakika mutu huyu ndiye Nabii aliyepaswa kuja!” Wengine wakasema: “Huyu ni Kristo.” Lakini wengine wakasema: “Basi Kristo angeweza kutokea Galilaya? Maandiko Matakatifu hayakusema kwamba Kristo atazaliwa katika ukoo wa mufalme Daudi na katika muji Betelehemu, pahali Daudi alipoishi?” Basi kukatokea mikorogano katika kundi juu ya Yesu. Wengine katikati yao walitaka kumufunga, lakini hakuna mutu aliyemukamata. Kisha wale walinzi wakarudi kwa wakubwa wa makuhani na Wafarisayo. Nao wakawauliza walinzi: “Sababu gani hamukuleta Yesu?” Walinzi wakajibu: “Hatujasikia mutu akisema sawasawa na mutu yule!” Basi Wafarisayo wakawauliza: “Na ninyi vilevile mumedanganywa? Ni nani kati ya wakubwa wetu au kati ya Wafarisayo aliyemwamini? Lakini watu hawa wasiojua Sheria ya Musa wamelaaniwa.” Nikodemo, yule aliyekuwa amemwendea Yesu mbele, alikuwa mumoja wa Wafarisayo waliokuwa pale. Akawaambia: “Kufuatana na Sheria, hatuwezi kumuhukumu mutu mbele ya kumusikiliza na kujua yale aliyofanya.” Wakamujibu: “Na wewe vilevile umetoka Galilaya? Uchunguze Maandiko Matakatifu, nawe utaona kwamba Galilaya hakutoki nabii.” [ Kisha kila mumoja akarudi kwake. Yesu vilevile akajiendea kwa mulima wa Mizeituni. Na kesho yake asubui mapema akarudi tena katika hekalu. Watu wote wakamufikia, naye alipoikaa, akaanza kuwafundisha. Halafu walimu wa Sheria pamoja na Wafarisayo wakaleta mbele yake mwanamuke mumoja aliyekamatwa katika uzinzi. Wakamusimamisha mbele ya watu wote na kumwambia Yesu: “Mwalimu, mwanamuke huyu amekamatwa akizini. Kufuatana na Sheria, Musa alituamuru kuwaua kwa mawe wanawake wa namna hii. Sasa, wewe unasema nini?” Wao walisema hivi kwa kumupima, kusudi wapate sababu ya kumushitaki. Lakini Yesu akainama na kuandika juu ya udongo kwa kidole chake. Nao walipozidi kumwuliza, Yesu akainuka na kuwaambia: “Mutu asiyekuwa na zambi kati yenu, akuwe wa kwanza kumutupia jiwe.” Kisha akainama tena na kuandika juu ya udongo. Wakati waliposikia maneno haya, wakaondoka wote mumoja kwa mumoja, wakianzia kwa wazee. Yesu akabaki pale peke yake pamoja na yule mwanamuke aliyekuwa akisimama mbele yake. Na Yesu alipoinuka, akamwuliza: “Mama, wale watu wako wapi sasa? Hakuna hata mumoja kwa kukuhukumu?” Mwanamuke yule akamujibu: “Bwana, hakuna mutu.” Basi Yesu akamwambia: “Mimi vilevile sikuhukumu. Ujiendee, lakini usifanye zambi tena.”] Yesu akawaambia watu tena: “Mimi ni mwangaza wa dunia. Yeye anayenifuata hatatembea katika giza hata kidogo, lakini atakuwa na mwangaza wa uzima.” Kwa hiyo Wafarisayo wakamwambia: “Ushuhuda wako si wa kweli, kwa kuwa unajishuhudia wewe mwenyewe.” Yesu akawajibu: “Hata nikijishuhudia mimi mwenyewe, ushuhuda wangu ni wa kweli, kwa sababu ninajua pahali nilipotoka na pahali ninapokwenda. Lakini ninyi hamujui pahali nilipotoka wala pahali ninapokwenda. Ninyi munahukumu kwa kufuatana na mafikiri ya kimutu; lakini mimi simuhukumu mutu. Lakini hata ningehukumu, hukumu yangu ingekuwa ya kweli, kwa sababu sihukumu peke yangu, lakini Baba aliyenituma ni pamoja nami. Na imeandikwa hata katika Sheria yenu kama ushuhuda wa watu wawili ni wa kweli. Ninajishuhudia mimi mwenyewe na Baba aliyenituma ananishuhudia vilevile.” Basi wakamwuliza: “Baba yako yuko wapi?” Yesu akajibu: “Hamunijui mimi wala hamumujui Baba yangu. Kama mungenijua mimi, mungemujua Baba yangu vilevile.” Yesu alisema maneno haya wakati alipokuwa akifundisha katika hekalu, kwenye sanduku za kuwekea matoleo. Hakuna mutu aliyemufunga, kwa sababu wakati wake ulikuwa haujatimia. Yesu akawaambia watu tena: “Mimi ninajiendea, nanyi mutanitafuta, lakini mutakufa katika zambi zenu. Na zaidi ya hii hamuwezi kufika pahali ninapokwenda.” Wakubwa wa Wayuda wakaulizana: “Yeye anasema kwamba hatuwezi kufika pahali anapokwenda; maana yake atakwenda kujiua?” Yesu akawajibu: “Ninyi munatoka hapa chini, lakini mimi nimetoka juu. Ninyi ni wa dunia hii, lakini mimi si wa dunia hii. Ni kwa sababu hii niliwaambia ninyi kama mutakufa katika zambi zenu. Musipoamini kwamba ‘Mimi Ndimi ’, hakika mutakufa katika zambi zenu.” Basi wakamwuliza: “Wewe ni nani?” Yesu akawajibu: “Mimi ni yule niliyewaambia tangu mwanzo. Nina maneno mengi ya kusema juu yenu na ya kuwahukumu. Lakini yule aliyenituma ni wa kweli, nami ninajulisha dunia maneno yale niliyosikia kwake.” Hawakujua kama alisema juu ya Baba yake. Halafu Yesu akawaambia: “Wakati mutakapomunyanyua Mwana wa Mutu juu, mutafahamu kwamba ‘Mimi Ndimi.’ Na zaidi ya hii mutatambua kwamba sifanyi neno lolote kwa mapenzi yangu, lakini ninasema tu yale niliyofundishwa na Baba. Yule aliyenituma ni pamoja nami; hakuniacha peke yangu, kwa sababu siku zote ninafanya maneno yanayomupendeza.” Alipokuwa akisema maneno haya, watu wengi wakamwamini. Basi Yesu akawaambia wale Wayuda waliomwamini: “Kama mukitii mafundisho yangu, ninyi ni wanafunzi wangu hakika. Halafu mutajua ukweli, na ukweli utawaweka huru.” Wakamujibu: “Sisi ni wa uzao wa Abrahamu, wala hatujakuwa watumwa wa mutu hata siku moja. Namna gani basi unaweza kutuambia kwamba tutapata uhuru?” Yesu akawajibu: “Kweli, kweli ninawaambia: kila mutu anayefanya zambi ni mutumwa wa zambi. Mutumwa hahesabiwi kuwa mumoja wa jamaa siku zote, lakini mwana anahesabiwa kuwa mumoja wa jamaa siku zote. Kama Mwana akiwapatia uhuru, basi mutapata uhuru wa kweli. Ninajua kwamba ninyi ni uzao wa Abrahamu. Lakini munatafuta kuniua, kwa sababu munakataa kukubali mafundisho yangu. Mimi ninasema yale niliyoona kwa Baba yangu, lakini ninyi munafanya yale muliyosikia kutoka kwa baba yenu.” Wakamujibu: “Baba yetu ni Abrahamu.” Yesu akawaambia: “Kama mungekuwa watoto wa Abrahamu, basi mungefanya matendo yale Abrahamu aliyofanya. Lakini sasa munatafuta kuniua ijapokuwa nimewaambia ukweli niliousikia kutoka kwa Mungu. Abrahamu hakufanya vile. Ninyi munafanya matendo yale baba yenu anayofanya.” Wakamujibu: “Sisi si watoto wa haramu. Tuko na baba mumoja, naye ndiye Mungu.” Yesu akawaambia: “Kama Mungu angekuwa Baba yenu, mungenipenda, kwa maana nimetoka kwa Mungu na sasa niko hapa. Sikukuja kwa mamlaka yangu mwenyewe, lakini yeye ndiye aliyenituma. Kwa sababu gani hamuelewi maneno ninayowaambia? Ni kwa sababu hamutaki kusikia maneno yangu. Baba yenu ni Shetani, nanyi munataka kutimiza sawa vile huyo baba yenu anavyotamani. Yeye ni mwuaji siku zote, naye hajasimama katika ukweli, kwa sababu ndani yake hakuna ukweli. Wakati anaposema uongo, masemi yake yanatokana na tabia yake, kwa sababu yeye ni mwongo na baba ya uongo. Na kwa ngambo yangu, ninyi hamuniamini kwa maana ninasema ukweli. Nani kati yenu anaweza kuhakikisha kwamba nimefanya zambi? Ikiwa ninasema ukweli, kwa sababu gani hamuniamini? Anayekuwa mutu wa Mungu anasikia maneno ya Mungu. Hamusikii, kwa sababu ninyi si watu wa Mungu.” Wayuda wakamujibu: “Sisi tulikuwa na haki ya kusema kwamba wewe ni Musamaria na kwamba uko na pepo.” Yesu akajibu: “Mimi sina pepo, lakini ninamuheshimu Baba yangu, nanyi munanikosea heshima. Mimi sijitafutii sifa yangu mwenyewe, lakini kuna mumoja anayeitafuta kwa ajili yangu, naye ndiye mwenye uwezo wa kuhukumu. Kweli, kweli ninawaambia: kama mutu akishika maneno yangu, hatakufa hata milele.” Halafu Wayuda wakamwambia: “Sasa tunajua hakika kwamba uko na pepo! Abrahamu amekufa, na manabii wamekufa vilevile, nawe unasema kwamba mutu akishika maneno yako, hatakufa hata milele. Wewe ni mukubwa kuliko babu yetu Abrahamu? Yeye alikufa, na manabii walikufa vilevile. Wewe unajiona kuwa nani?” Yesu akajibu: “Kama nikijitafutia sifa yangu mwenyewe, sifa ile haina maana. Baba yangu ndiye anayenisifu, yule munayejidai kwamba ni Mungu wenu! Ninyi hamumujui, lakini mimi ninamujua. Kama ningesema kwamba simujui, ningekuwa mwongo kama ninyi. Lakini ninamujua na ninashika neno lake. Baba yenu Abrahamu alishangilia akitumainia kuona siku ya kuja kwangu; na wakati alipoiona, alifurahi.” Halafu Wayuda wakamwambia: “Wewe haujaeneza umri wa miaka makumi tano, nawe umemwona Abrahamu?” Yesu akawajibu: “Kweli, kweli ninawaambia: mbele Abrahamu hajazaliwa, mimi nilikuwa niko.” Kwa ajili ya hii, wakaokota mawe kwa kumutupia. Lakini Yesu akajificha na kutoka ndani ya hekalu. Yesu alipokuwa akipita katika njia, akaona mutu mumoja aliyekuwa kipofu tangu kuzaliwa kwake. Wanafunzi wake wakamwuliza: “Mwalimu, kwa sababu gani mutu huyu alizaliwa kipofu? Ni kwa ajili ya malipizi ya zambi yake mwenyewe au zambi ya wazazi wake?” Yesu akajibu: “Mutu huyu hakuzaliwa kipofu kwa ajili ya zambi yake wala zambi ya wazazi wake. Lakini amekuwa hivi kusudi matendo ya Mungu yaonekane kwa njia yake. Imetupasa kufanya kazi za yule aliyenituma wakati kungali muchana, kwa sababu usiku unakaribia, wakati mutu asipoweza kutumika. Wakati nikingali katika dunia, mimi ni mwangaza wa dunia.” Yesu alipokwisha kusema vile, akatema mate chini, akayavuruga pamoja na mavumbi na kufanya matope kidogo, akayapakaa kwa macho ya yule kipofu na kumwambia: “Kwenda unawe uso katika kisima cha Siloamu” (maana ya jina hili ni “Aliyetumwa”). Basi yule kipofu akaenda na kunawa uso, akarudi akiwa mwenye kuona. Jirani zake na wale waliomwona zamani akiwa mwenye kuombaomba, wakasema: “Si mutu huyu ndiye yule aliyekuwa akiikaa chini na kuombaomba?” Wamoja wakasema: “Ni yeye.” Lakini wengine wakasema: “Hapana, si yeye, anafanana naye tu.” Lakini yeye mwenyewe akasema: “Ni mimi.” Basi wakamwuliza: “Macho yako yaliponyeshwa namna gani?” Akajibu: “Mutu yule anayeitwa Yesu alifanya matope kidogo na kuyapakaa kwa macho yangu, na kuniambia kwamba niende kunawa uso katika kisima cha Siloamu. Nami nikaenda, nikanawa, na halafu nikapata kuona.” Nao wakamwuliza tena: “Yule mutu yuko wapi?” Akajibu: “Sijui.” Wakamupeleka yule mutu aliyekuwa kipofu kwa Wafarisayo. Na siku ile Yesu alipofanya matope na kuponyesha macho ya mutu yule, ilikuwa siku ya Sabato. Kwa hiyo Wafarisayo nao wakamwuliza namna gani alivyopata kuona. Naye akawaambia: “Alinipakaa matope kidogo kwa macho, nami nikanawa uso na sasa ninaona.” Wafarisayo wamoja wakasema: “Mutu huyu hakutoka kwa Mungu kwa sababu hashiki sheria ya siku ya Sabato.” Lakini wengine wakasema: “Mutu mwenye zambi anaweza kuonyesha kitambulisho kama hiki?” Basi kukatokea mikorogano kati yao. Wafarisayo wakamwuliza tena yule aliyekuwa kipofu: “Na wewe unasema nini juu ya yule aliyekuponyesha macho?” Akajibu: “Yeye ni nabii.” Lakini wakubwa wa Wayuda hawakusadiki kama alikuwa kipofu na kwamba alikuwa sasa akiona mpaka walipowaita wazazi wake na kuwauliza: “Huyu ndiye mwana wenu munayesema kama alizaliwa kipofu? Namna gani anaona?” Wazazi wake wakawajibu: “Tunajua hakika kwamba huyu ni mwana wetu na kwamba alizaliwa kipofu. Lakini hatujui kilichotokea hata anaona sasa, wala hatujui ni nani aliyemuponyesha macho. Yeye ni mutu muzima. Mumwulize yeye mwenyewe, naye atawaelezea maneno yake.” Wazazi wake walisema hivi kwa sababu waliogopa wakubwa wa Wayuda. Wakubwa wale walikuwa wamekwisha kupatana kwamba mutu yeyote anayesadiki kuwa Yesu ndiye Kristo, atatengwa asiingie katika nyumba ya kuabudia. Na hiyo ndiyo sababu wazazi wake walisema kwamba yeye ni mutu muzima, wamwulize. Halafu wakubwa wa Wayuda wakamwita yule aliyekuwa kipofu kwa mara ya pili na kumwambia: “Sema ukweli mbele ya Mungu! Kwa ngambo yetu tunajua kwamba mutu yule ni mwenye zambi.” Yeye akajibu: “Kama yeye ni mwenye zambi, mimi sijui. Neno moja ninalojua ni kwamba mimi nilikuwa kipofu na sasa ninaona.” Wakamwuliza tena: “Yeye alikufanyia nini? Namna gani alikuponyesha macho?” Naye akawajibu: “Nimekwisha kuwaelezea lakini hamupendi kusikia. Kwa sababu gani munataka niwaambie tena? Ninyi vilevile munataka kuwa wanafunzi wake?” Wakamutukana, wakimwambia: “Wewe ndiwe mwanafunzi wa mutu yule! Sisi ni wanafunzi wa Musa. Tunajua kwamba Mungu alisema na Musa, lakini hatujui pahali mutu yule anapotoka!” Naye akawajibu: “Kweli neno hili ni la kushangaza kusema kwamba hamujui pahali alipotoka, ijapokuwa ameniponyesha macho. Tunajua kwamba Mungu hasikilizi maombi ya wenye zambi, lakini anamusikiliza mutu yule anayemuheshimu na kufanya sawa anavyotaka. Hatujasikia wakisema hata siku moja kwamba kuna mutu aliyeponyesha macho ya mutu aliyezaliwa kipofu. Kama mutu huyu asingetoka kwa Mungu, hangeweza kufanya kitu.” Wakamujibu: “Wewe, uko mwenye zambi kabisa tangu kuzaliwa kwako! Unataka kutufundisha?” Halafu wakamufukuza inje. Yesu akapata habari kwamba yule aliyekuwa kipofu amefukuzwa. Yesu alipokutana naye, akamwuliza: “Unamwamini Mwana wa Mutu?” Yule mutu akamujibu: “Bwana, unielezee yeye ni nani, kusudi nipate kumwamini.” Yesu akamwambia: “Umemwona, na ni yeye anayesema nawe sasa.” Basi yule mutu akasema: “Bwana, ninaamini.” Naye akamwabudu Yesu. Kisha Yesu akasema: “Nimekuja katika dunia kusudi hukumu ipate kufanyika; maana yake vipofu wapate kuona, nao wanaoona wapate kuwa vipofu.” Wafarisayo wamoja waliokuwa pamoja naye waliposikia maneno haya, wakamwuliza: “Ni kusema sisi ni vipofu vilevile?” Yesu akawajibu: “Mungekuwa vipofu, hamungekuwa na zambi. Lakini kwa maana munajidai kwamba munaona, mungali katika zambi.” Yesu akasema: “Kweli, kweli ninawaambia: mutu asiyeingia kwa mulango wa upango wa kondoo, lakini anapandia na kuingilia nafasi ingine, yeye ni mwizi na munyanganyi. Lakini anayeingia kwa mulango ni muchungaji wa kondoo. Zamu anamufungulia mulango na kondoo wanasikia sauti yake. Naye anawaita kondoo wake kila mumoja kwa jina lake na kuwapeleka inje. Anapokwisha kuwatia hao kondoo wake inje, anawatangulia, nao wanamufuata kwa sababu wanajua sauti yake. Kondoo wale hawawezi kumufuata mugeni; lakini watamukimbia, kwa sababu hawajui sauti ya mugeni.” Yesu aliwaambia mufano huu, lakini hawakuelewa maneno aliyosema. Basi Yesu akaongeza kusema: “Kweli, kweli ninawaambia: mimi ni mulango wa upango wa kondoo. Wote waliokuja mbele sijafika ni wizi na wanyanganyi; lakini kondoo hawakuwasikia. Mimi ni mulango. Mutu akiingia kwa kupitia kwangu, ataokoka, ataingia na kutoka, naye atapata chakula. Mwizi anakuja tu kwa kuiba, kuua na kuharibu. Mimi nimekuja kusudi watu wapate uzima, ndio uzima wa kweli kabisa. “Mimi ni muchungaji mwema. Muchungaji mwema anatoa maisha yake kwa ajili ya kondoo wake. Lakini mutumishi wa mushahara si muchungaji, wala kondoo si wake. Kwa sababu hii wakati anapoona imbwa wa pori anakuja, anaacha kondoo na kukimbia. Na halafu imbwa wa pori anawakamata na kuwasambaza. Yeye hashuguliki na kondoo kwa sababu anatumikia mushahara tu. Mimi ni muchungaji mwema. Ninajua kondoo wangu na kondoo wangu wananijua, kama vile Baba anavyonijua mimi, na mimi ninavyomujua Baba. Vilevile mimi ninatoa maisha yangu kwa ajili ya kondoo wangu. Niko na kondoo wengine wasiokuwa wa kundi hili. Ninapaswa vilevile kuwaleta, nao watasikia sauti yangu, na kutakuwa kundi moja na muchungaji mumoja. “Baba ananipenda kwa sababu mimi mwenyewe ninajitoa kufa, kusudi nipate kuwa muzima tena. Hakuna mutu anayeweza kunionodoa uzima, lakini ninajitoa mwenyewe kufa kwa mapenzi yangu. Niko na uwezo wa kujitoa kufa na niko na uwezo wa kuwa tena muzima. Ni vile Baba yangu alivyoniagiza kufanya.” Kwa sababu ya maneno haya kukatokea tena mikorogano kati ya Wayuda. Wengi kati yao wakasema: “Yuko na pepo! Kweli ni mwenda-wazimu! Sababu gani munamusikiliza?” Lakini wengine wakasema: “Mutu anayekuwa na pepo hawezi kusema hivi. Pepo zinaweza kuponyesha macho ya vipofu?” Siku moja, katika nyakati za mvua kubwa, kukakuwa sikukuu ya Kukumbuka Muzinduo wa hekalu katika Yerusalema. Yesu alikuwa akitembea ndani ya hekalu katika baraza iliyoitwa baraza ya Solomono. Halafu Wayuda wakamuzunguka, na kumwambia: “Mpaka wakati gani utatuzungusha kichwa? Kama wewe ni Kristo, utuambie waziwazi.” Yesu akawajibu: “Nimekwisha kuwaambia ninyi, lakini hamusadiki. Matendo ninayofanya kwa mamlaka ya Baba yananishuhudia mimi. Lakini ninyi hamusadiki kwa sababu ninyi si kondoo wangu. Kondoo wangu wanasikia sauti yangu, ninawajua, nao wananifuata. Mimi ninawapa uzima wa milele, nao hawatapotea hata milele, wala hakuna mutu anayeweza kuwanyanganya toka katika mukono wangu. Baba yangu aliyenipa kondoo hawa ni mukubwa kuliko wote, na hakuna mutu anayeweza kuwanyanganya toka kwa Baba yangu. Mimi na Baba yangu tuko mumoja.” Halafu Wayuda wakaokota tena mawe kwa kumutupia. Yesu akawaambia tena: “Nimewaonyesha matendo mengi mazuri kwa uwezo wa Baba. Ni kwa sababu ya tendo gani kati ya hayo munataka kunitupia mawe?” Wayuda wakamujibu: “Hatutaki kukutupia mawe kwa ajili ya tendo zuri, lakini kwa sababu unamutukana Mungu. Wewe ni mutu tu, lakini unajifanya kuwa Mungu!” Yesu akawajibu: “Imeandikwa katika sheria yenu kwamba Mungu amesema: ‘Ninyi ni miungu.’ Maandiko Matakatifu hayawezi kuvunjwa. Mungu aliwaita ‘miungu’ wale walioambiwa neno lake. Kwa upande wangu, nilichaguliwa na Mungu na kutumwa naye katika dunia. Basi namna gani munasema kwamba ninamutukana Mungu kwa sababu nilisema kwamba mimi ni Mwana wa Mungu? Kama sifanyi matendo ambayo Baba yangu ananiamuru, musiniamini. Lakini kama nikiyatenda, hata ikiwa hamuniamini mimi, basi mwamini matendo yangu, kusudi mupate kujua kabisa kwamba mimi na Baba ni mumoja, yeye ni ndani yangu, nami ndani yake.” Wakajaribu tena kumufunga Yesu, lakini akawaponyoka. Halafu Yesu akaenda tena ngambo ingine ya Yordani, pahali Yoane alipobatiza watu zamani, na kubaki kule. Watu wengi wakamufikia na kusema: “Yoane hakuonyesha hata kitambulisho kimoja, lakini maneno yote aliyoyasema juu ya mutu huyu yalikuwa ya kweli.” Na kule watu wengi wakamwamini Yesu. Kulikuwa mutu mumoja aliyeitwa Lazaro, muzaliwa wa Betania aliyepatwa na ugonjwa. Wadada zake Maria na Marta walikaa katika kijiji kile. (Huyu Maria ndiye yule aliyemupakaa Bwana marasi na kupanguza miguu yake na nywele zake, na ni Lazaro kaka yake ndiye alikuwa mugonjwa.) Hawa wadada wawili wakatuma habari hii kwa Yesu: “Bwana, rafiki yako mupendwa ni mugonjwa.” Wakati Yesu aliposikia habari hii, akasema: “Tukio la ugonjwa huu si la kumwua, lakini shabaha yake ni kuonyesha utukufu wa Mungu na kusudi Mwana wa Mungu atukuzwe.” Yesu aliwapenda Marta na dada yake pamoja na Lazaro. Yesu aliposikia kwamba Lazaro yuko mugonjwa, akabaki tena kwa muda wa siku mbili pahali alipokuwa. Kisha akawaambia wanafunzi wake: “Turudi Yudea.” Wanafunzi wakamwambia: “Mwalimu, hakujapita siku nyingi tokea pale Wayuda walipotaka kukutupia mawe, na sasa unataka kwenda tena kule!” Yesu akajibu: “Katika muchana kuna saa kumi na mbili. Kama mutu akitembea wakati wa muchana hajikwai, kwa sababu anaona mwangaza wa dunia hii. Lakini kama mutu akitembea usiku, anajikwaa, kwa sababu hana mwangaza ndani yake.” Yesu alipokwisha kusema maneno haya, akaongeza kuwaambia: “Rafiki yetu Lazaro amelala usingizi, lakini ninakwenda kumwamusha.” Basi wanafunzi wake wakamujibu: “Bwana, ikiwa amelala usingizi, atapona.” Yesu alikuwa akisema kwamba Lazaro amekufa, lakini wanafunzi wake walizani kwamba amesema juu ya kulala usingizi. Basi Yesu akawaambia waziwazi: “Lazaro amekufa. Nami ninafurahi kwa ajili yenu, kwa sababu sikukuwa kule, kusudi mupate kuamini. Tuende kule anapokuwa.” Basi Toma, anayeitwa “Pacha,” akawaambia wanafunzi wenzake: “Nasi tuende vilevile, tukufie pamoja naye.” Wakati Yesu alipofika, akamukuta Lazaro amekwisha kuzikwa tangu siku ine. Kati ya kijiji cha Betania na Yerusalema kulikuwa umbali yapata kilometre tatu. Wayuda wengi walikuwa wamekuja kwa Marta na Maria kwa kuwafariji kwa ajili ya kifo cha kaka yao. Marta aliposikia kama Yesu anakuja, akaenda kumupokea katika njia, lakini Maria alibaki ndani ya nyumba. Marta akamwambia Yesu: “Bwana, kama ungekuwa hapa, kaka yangu hangekufa. Lakini ninajua kwamba hata sasa, kitu chochote utakachomwomba Mungu, atakupa.” Yesu akamwambia: “Kaka yako atafufuka.” Marta akajibu: “Ninajua kwamba atafufuka wakati watu watakapofufuka siku ya mwisho.” Yesu akamwambia: “Mimi ni ufufuko na uzima, kwa maana anayeniamini, ataishi tena hata ikiwa amekufa. Vilevile yeyote anayeishi ndani yangu na kuniamini, hatakufa hata milele. Unaamini maneno haya?” Akamujibu: “Ndiyo, Bwana, ninaamini kwamba wewe ni Kristo, Mwana wa Mungu, yule aliyepaswa kuja katika dunia.” Marta alipokwisha kusema maneno hayo, akaenda kumwita dada yake Maria na kumwambia kwa siri: “Mwalimu amekuja, na anakuita.” Wakati Maria aliposikia hivi, akaondoka upesi kwenda kumukuta. (Yesu alikuwa hajaingia bado katika kijiji, alikuwa angali pahali Marta alipomukuta.) Wakati wale Wayuda waliokuwa ndani ya nyumba pamoja na Maria kwa kumufariji walipomwona akisimama upesi na kutoka, wakamufuata. Walizani kama anakwenda kulia kwenye kaburi. Maria alipofika pale Yesu alipokuwa na kumwona, akaanguka kwenye miguu yake na kusema: “Bwana, kama ungekuwa hapa, kaka yangu hangekufa.” Wakati Yesu alipomwona akilia, na wale Wayuda waliokuja pamoja naye wakilia vilevile, akasisimua kwa huzuni nyingi na kufazaika. Akauliza: “Mulimuzika wapi?” Wakamujibu: “Bwana, kuja uone.” Yesu akatoa machozi. Halafu Wayuda wamoja wakasema: “Angalia namna alivyomupenda kweli!” Lakini wengine kati yao wakasema: “Yeye aliyeponyesha kipofu, asingeweza kuzuia mutu huyu asikufe?” Basi Yesu akasisimua tena kwa huzuni, na kwenda kwenye kaburi. Kaburi lile lilikuwa pango lililofungwa na jiwe kubwa. Yesu akasema: “Muondoshe jiwe hili!” Marta, dada wa yule marehemu, akamujibu: “Bwana, anaanza sasa kunuka, kwa maana ni siku ine sasa tangu alipozikwa!” Yesu akamwambia: “Sikukuambia kwamba ukiamini utaona utukufu wa Mungu?” Basi wakaondosha lile jiwe. Yesu akainua macho juu, akasema: “Baba, ninakushukuru kwa sababu umenisikia. Na ninajua kwamba unanisikia siku zote, lakini ninasema hivi kwa sababu ya watu hawa wanaokusanyika hapa kusudi wapate kuamini kwamba wewe ndiwe uliyenituma.” Wakati alipokwisha kusema maneno haya, akaita kwa sauti kubwa, akisema: “Lazaro, toka inje.” Halafu yule marehemu akatoka inje, akiwa amefungwa mikono na miguu kwa vitambaa, na uso wake ukifunikwa na nguo. Yesu akawaambia: “Mumufungue, mumwache ajiendee.” Wayuda wengi kati ya wale waliokuja kwa Maria, na walioona mambo Yesu aliyofanya, wakamwamini. Lakini wengine kati yao wakawaendea Wafarisayo na kuwaambia mambo Yesu aliyofanya. Basi wakubwa wa makuhani na Wafarisayo wakakusanya Baraza yao Kubwa, na kusema: “Tufanye nini kwa kuona mutu huyu anaonyesha vitambulisho vingi? Kama tukimwachilia kuendelea hivi, watu wote watamwamini, nao Waroma watakuja kuharibu hekalu letu na taifa letu!” Halafu mumoja kati yao, jina lake Kayafa, aliyekuwa Kuhani Mukubwa mwaka ule, akasema: “Hamujui kitu, ninyi! Hamufahamu kwamba ni afazali mutu mumoja akufe kwa ajili ya watu, kuliko taifa zima kuangamizwa?” (Yeye hakusema maneno haya kutokana na mawazo yake mwenyewe; lakini kwa maana yeye ndiye aliyekuwa Kuhani Mukubwa mwaka ule, alitabiri kwamba Yesu atakufa kwa ajili ya taifa la Wayuda. Na kufa kwake si kwa ajili ya taifa hili tu, lakini vilevile kwa ajili ya watoto wa Mungu waliosambazwa, kusudi apate kuwaunga katika umoja.) Basi tangia siku ile wakakusudia kumwua Yesu. Kwa sababu hii Yesu hakutembea tena akijionyesha waziwazi kati ya Wayuda. Kisha akajiendea pamoja na wanafunzi wake katika inchi iliyokuwa karibu na jangwa katika muji unaoitwa Efuraimu. Nao wakabaki kule. Sikukuu ya Wayuda ya Pasaka ilikuwa karibu. Basi watu wengi toka katika vijiji wakaenda Yerusalema kusudi wajitakase mbele ya Pasaka. Wakamutafuta Yesu, na wakaulizana hivi ndani ya hekalu: “Munawaza nini? Atakuja kwa karamu au hapana?” Nao wakubwa wa makuhani na Wafarisayo walikuwa wametoa amri kwamba mutu akijua pahali Yesu alipokuwa, alete habari kusudi wapate kumufunga. Siku sita mbele ya Pasaka, Yesu alifika Betania, kwao Lazaro, yule mutu Yesu aliyemufufua. Kule wakamutayarishia chakula cha magaribi. Marta aliwashugulikia, na Lazaro alikuwa mumoja wa wale waliokula pamoja na Yesu. Halafu Maria akatwaa nusu ya litre ya marasi ya bei kali, yaliyotengenezwa na maua ya nardo safi. Akaipakaa kwa miguu ya Yesu na kuipanguza na nywele zake. Nyumba yote ikajaa harufu ya marasi. Lakini Yuda Iskariota, mumoja wa wanafunzi wa Yesu, yule atakayemutoa, akasema: “Kwa sababu gani marasi hii ya bei kali haikuuzishwa kwa bei ya vikoroti mia tatu vya feza na kuwagawanyia wamasikini mali ile?” (Hakusema maneno haya kwa sababu aliwasikilia wamasikini huruma, lakini kwa sababu alikuwa mwizi. Ni yeye aliyekuwa akichunga mufuko wa feza, naye alikuwa akijitwalia mali toka ndani yake.) Lakini Yesu akasema: “Umwache kimya, kwa maana alikuwa ameweka marasi hii kwa ajili ya siku ya maziko yangu. Mutakuwa na wamasikini pamoja nanyi siku zote, lakini hamutakuwa nami siku zote.” Kundi kubwa la Wayuda wakapata habari kwamba Yesu yuko Betania. Kwa hiyo wakaenda kule, si kwa sababu ya Yesu tu, lakini vilevile kwa kumwona Lazaro aliyefufuliwa naye. Basi wakubwa wa makuhani wakakata shauri la kumwua Lazaro vilevile, kwa maana kwa ajili yake Wayuda wengi walijitenga nao na kumwamini Yesu. Kesho yake lile kundi kubwa la watu waliofika kwa sikukuu ya Pasaka wakasikia kwamba Yesu alikuwa katika njia kuja Yerusalema. Basi wakatwaa matawi ya ngazi na kwenda kumupokea, wakilalamika kwa sauti kubwa, wakisema: “Mungu asifiwe! Abarikiwe huyu anayekuja kwa jina la Bwana! Abarikiwe mufalme wa Waisraeli!” Yesu akapata mwana-punda na kupanda juu yake, kama vile inavyosemwa katika Maandiko haya Matakatifu: “Musiogope ninyi wakaaji wa Sayuni! Angalia, mufalme wenu anakuja, akipanda juu ya mwana-punda.” Wanafunzi wake hawakuelewa maneno haya kwanza, lakini wakati Yesu alipokwisha kutukuzwa, wakakumbuka kwamba maneno haya yameandikwa juu yake na ni vile walivyomutendea. Wale watu wote waliokuwa pamoja na Yesu wakati alipomwita Lazaro toka ndani ya kaburi na kumufufua walishuhudia mambo yaliyofanyika. Kwa sababu hii watu wengi walikwenda kumupokea, kwa maana walikuwa wamesikia kwamba ameonyesha kitambulisho hicho. Basi Wafarisayo wakasemezana hivi: “Hamwoni kwamba hatuwezi kufanya kitu? Angalia, dunia nzima inamufuata!” Kulikuwa Wagriki wamoja kati ya wale watu waliofika Yerusalema kuabudu wakati wa sikukuu. Basi wakamwendea Filipo wa kijiji cha Betesaida ya Galilaya na kumwambia: “Bwana, tunataka kuonana na Yesu.” Filipo akaenda kumwambia Andrea, na kisha wote wawili wakaenda kumwelezea Yesu. Yesu akawajibu: “Saa ya kutukuzwa kwa Mwana wa Mutu imetimia. Kweli, kweli, ninawaambia: punje ya ngano inabaki peke yake tu, isipokuwa kama yenye kufa na kuzikwa ndani ya udongo. Lakini kama ikiwa yenye kufa, inatoa matunda mengi. Anayependelea maisha yake atayapoteza, lakini asiyeyashugulikia katika dunia hii, atayachunga hata atakapopata uzima wa milele. Kama mutu akitaka kunitumikia, anapaswa kunifuata, na hivi mutumishi wangu atakuwa popote nitakapokuwa. Mutu akinitumikia, Baba yangu atamupa heshima. “Sasa roho yangu inafazaika. Nami sijui niseme nini. Nimwombe Baba, aniokoe toka mambo yale yatakayofika saa hii? Hapana, kwa sababu nimefika kwa ajili ya yale yatakayofanyika saa hii. Baba, utukuze jina lako!” Halafu sauti ikasikilika toka mbinguni ikisema: “Nimelitukuza, nami nitalitukuza tena.” Kundi la watu waliosimama pale na waliosikia sauti ile wakasema: “Ile ilikuwa ngurumo ya radi!” Wengine wakasema: “Ni malaika aliyekuwa akisema naye!” Lakini Yesu akawaambia: “Sauti hii haikusikilika kwa ajili yangu, lakini kwa ajili yenu. Sasa ni wakati wa dunia hii kuhukumiwa; sasa mutawala wa dunia hii atashindwa. Lakini mimi, nitakaponyanyuliwa toka katika dunia, nitawavuta watu wote kuja kwangu.” (Alisema hivi kwa kuonyesha ni kifo gani atakachokufa.) Na lile kundi la watu wakamujibu: “Sisi tumesikia katika maandiko ya Sheria kwamba Kristo ataishi milele. Basi namna gani unaweza kusema kama Mwana wa Mutu anapaswa kunyanyuliwa juu? Na huyu Mwana wa Mutu ni nani?” Yesu akawaambia: “Mwangaza ungali kati yenu kwa muda kidogo. Mutembee wakati mungali na mwangaza, kusudi giza lisiwafunike, kwa sababu anayetembea katika giza hajui pahali anapokwenda. Basi muaminie mwangaza ule wakati mungali nao, kusudi mukuwe watu wa mwangaza.” Yesu alipokwisha kusema maneno hayo, akajiendea na kujificha mbali na lile kundi. Ingawa vitambulisho vyote alivyoonyesha mbele yao, hawakumwamini, kusudi maneno haya yaliyosemwa na nabii Isaya yatimie: “Bwana, ni nani aliyeamini habari tuliyopasha? Nani aliyefunuliwa matendo ya uwezo ya Bwana?” Hawangeweza vilevile kuamini, kufuatana na maneno haya Mungu aliyomwambia Isaya tena: “Mungu amepofusha macho yao, kusudi yasipate kuona. Ameifanya mioyo yao kuwa migumu, wala wasipate kunigeukia nami ningewaponyesha.” Isaya alisema maneno haya kwa sababu aliona kwa mbali utukufu wa Yesu, naye alisema habari zake. Hata hivi wengi kati ya wakubwa wa Wayuda wakamwamini Yesu. Lakini kwa sababu ya Wafarisayo, hawakushuhudia kwamba wameamini. Waliogopa kwamba watatengwa wasiingie katika nyumba ya kuabudia. Wao walipenda kusifiwa na watu kuliko kupata sifa inayotoka kwa Mungu. Halafu Yesu akasema hivi kwa sauti: “Anayeniamini haniamini mimi tu, lakini anamwamini vilevile yule aliyenituma. Anayeniona amemwona vilevile yule aliyenituma. Mimi nimekuja katika dunia kama mwangaza, kusudi mutu yeyote anayeniamini asikae katika giza. Mutu akisikia maneno yangu pasipo kuyashika, si mimi nitakayemuhukumu. Kwa maana sikukuja kuhukumu dunia, lakini nilikuja kuiokoa. Yule anayenikataa na asiyekubali maneno yangu atahukumiwa kufuatana nayo. Ni lile neno nililosema ndilo litakalomuhukumu siku ya mwisho. Kwa maana sikusema kwa mamlaka yangu mwenyewe, lakini Baba aliyenituma ndiye aliyeniagiza maneno nitakayosema na kuyafundisha. Nami ninajua kama amri yake inaleta uzima wa milele. Ni kwa hiyo maneno ninayosema, ninayasema tu kama vile Baba alivyoniagiza.” Kulikuwa kumebaki siku moja mbele ya kutimia kwa sikukuu ya Pasaka. Yesu alijua kwamba saa yake ya kutoka katika dunia na kurudi kwa Baba yake imetimia. Yeye alikuwa akiwapenda watu wake waliokuwa katika dunia, na akaendelea kuwapenda mpaka mwisho. Wakati Yesu na wanafunzi wake walipokuwa wakikula chakula cha magaribi, Shetani alikuwa amekwisha kumushawishi Yuda mwana wa Simoni Iskariota kwamba amutoe Yesu. Yesu alijua kwamba Baba yake ameweka vitu vyote chini ya mamlaka yake, na kwamba yeye mwenyewe alitoka kwa Mungu na anarudi kwa Mungu. Basi Yesu akaondoka kwenye chakula, akavua kanzu yake, akajifunga kitambaa katika kiuno. Kisha akatia maji ndani ya bakuli, na kuanza kunawisha miguu ya wanafunzi wake na kuipanguza na kile kitambaa alichokifunga katika kiuno. Alipofika kwenye Simoni Petro, Petro akamwambia: “Bwana, ni kweli wewe utaninawisha miguu?” Yesu akamujibu: “Sasa hauelewi jambo ninalofanya, lakini utalielewa nyuma.” Petro akamwambia: “Hautanawisha miguu yangu hata kidogo!” Yesu akamujibu: “Nisipokunawisha miguu, hauna ushirika pamoja nami.” Simoni Petro akamwambia tena: “Basi Bwana, ikiwa ni vile usininawishe miguu tu, lakini uninawishe mikono na kichwa vilevile.” Yesu akamwambia: “Aliyekwisha kuoga hahitaji kunawa tena, isipokuwa miguu yake tu, kwa maana mwili wake wote ni safi. Na ninyi ni safi, lakini si wote.” (Yesu alijua yule atakayemutoa; ndiyo maana alisema: “Ninyi wote si safi.”) Yesu alipokwisha kuwanawisha miguu, akavaa tena kanzu yake na kurudi kukaa kwenye chakula. Naye akawauliza: “Munaelewa jambo nililowafanyia? Munaniita ‘Mwalimu’ na ‘Bwana,’ na munasema kweli, maana ni vile ninavyokuwa. Basi kama mimi ninayekuwa Bwana na Mwalimu wenu nimewanawisha miguu, ninyi vilevile munapaswa kunawishana miguu. Mimi nimewapa ninyi mufano, mufanye sawasawa nilivyowafanyia. Kweli, kweli ninawaambia: mutumishi si mukubwa kuliko bwana wake, wala mujumbe si mukubwa kuliko yule aliyemutuma. Sasa kwa kuona munajua jambo hili, mutakuwa wenye heri kama mukilifanya. “Sisemi juu ya ninyi wote; ninawajua wale niliowachagua. Lakini inafaa maneno haya yanayosemwa na Maandiko Matakatifu yatimie: ‘Yule aliyechangia chakula nami, amenigeuka.’ Ninawaambia ninyi sasa hayo yote mbele hayajatokea, kusudi wakati yatakapotokea, mwamini kwamba ‘Mimi Ndimi.’ Kweli, kweli ninawaambia: mutu anayemupokea yule ninayemutuma, ananipokea mimi vilevile; na mutu anayenipokea, anamupokea yule aliyenituma.” Yesu alipokwisha kusema maneno hayo, akafazaika na kusema: “Kweli, kweli ninawaambia, mumoja wenu atanitoa.” Wanafunzi wakaangaliana, kwa maana hawakujua ni nani Yesu aliyemusema. Na kulikuwa mumoja wa wanafunzi ambaye Yesu alimupenda, na aliyekuwa akimwegamia Yesu pale kwenye chakula. Basi Simoni Petro akamukonyezea yule mwanafunzi jicho kusudi amwulize Yesu ni nani anayemusema. Halafu yule mwanafunzi akamwegamia Yesu na kumwuliza: “Bwana, ni nani?” Yesu akajibu: “Nitachovya kipande cha mukate. Yule nitakayemupa kipande kile ndiye yeye.” Basi Yesu akachovya kipande cha mukate na kumupa Yuda mwana wa Simoni Iskariota. Yuda alipokwisha kukamata kile kipande cha mukate, Shetani akamwingilia. Basi Yesu akamwambia: “Unayotaka kufanya, uyafanye upesi!” (Hakuna mutu kati ya wale waliokaa kwenye chakula aliyefahamu sababu gani Yesu alimwambia vile. Wamoja walizani kama Yesu amemwambia aende kununua vitu walivyohitaji kwa sikukuu, au aende kuwasaidia wamasikini, kwa sababu Yuda ndiye aliyekuwa akichunga mufuko wa feza.) Wakati Yuda alipokwisha kukamata kile kipande cha mukate, mara moja akatoka inje. Usiku ulikuwa umeingia. Wakati Yuda alipokwisha kutoka, Yesu akasema: “Sasa Mwana wa Mutu ametukuzwa, na Mungu ametukuzwa kwa njia yake. Na ikiwa Mungu ametukuzwa kwa njia yake, basi Mungu vilevile atamutukuza Mwana kwa njia yake mwenyewe, naye atamutukuza bila kukawia. Watoto wangu, ningali pamoja nanyi kwa muda mufupi tu. Mutanitafuta, lakini sawasawa nilivyowaambia Wayuda, ninawaambia ninyi vilevile kwamba hamuwezi kufika pahali ninapokwenda. Ninawapa amri mupya: mupendane ninyi kwa ninyi. Kama mimi nilivyowapenda, nanyi mupendane vilevile. Watu wote watajua kwamba ninyi ni wanafunzi wangu, ikiwa munapendana ninyi kwa ninyi.” Simoni Petro akamwuliza: “Bwana, unakwenda wapi?” Yesu akamujibu: “Hauwezi kunifuata sasa pahali ninapokwenda, lakini utanifuata nyuma.” Petro akamwuliza: “Bwana, sababu gani siwezi kukufuata sasa? Mimi ni tayari kutoa maisha yangu kwa ajili yako!” Yesu akamujibu: “Hakika wewe ni tayari kutoa maisha yako kwa ajili yangu? Kweli, kweli ninakuambia: mbele jogoo hajawika, utakuwa umekwisha kunikana mara tatu.” Yesu akawaambia wanafunzi wake: “Musifazaike; mumwamini Mungu, na muniamini mimi vilevile. Ndani ya nyumba ya Baba yangu kuna nafasi nyingi za kukaa. Isingekuwa hivi singewaambia kwamba ninakwenda kuwatayarishia nafasi. Nami nitakapokwisha kuwatayarishia ninyi nafasi, nitarudi tena na kuja kuwatwaa, kusudi pahali nitakapokuwa, ninyi mupate kuwa pale vilevile. Munajua njia ya kufika pahali ninapokwenda.” Toma akamwambia: “Bwana, hatujui pahali unapokwenda, basi namna gani tutajua njia?” Yesu akamujibu: “Mimi ni njia, ukweli na uzima. Mutu hawezi kufika kwa Baba asipopitia kwangu. Kama mungenijua mimi, mungemujua Baba yangu vilevile. Na tangu sasa mumemujua, na mumemwona.” Filipo akamwambia: “Bwana, utuonyeshe Baba, na ile itatutoshelea.” Yesu akajibu: “Filipo, nimekwisha kuwa nanyi siku nyingi sasa, nawe haujanijua bado? Aliyeniona mimi amemwona Baba. Basi sababu gani unasema: ‘Utuonyeshe Baba?’ Hauamini kwamba mimi na baba ni mumoja, yeye ni ndani yangu na mimi ndani yake? Maneno ninayowaambia siyasemi kwa mamlaka yangu mwenyewe, lakini Baba anayekaa ndani yangu ndiye anayefanya kazi zake. Muniamini wakati ninaposema kama mimi ni ndani ya Baba na Baba ni ndani yangu. Kama si vile, mwamini kwa sababu ya matendo niliyofanya. Kweli, kweli ninawaambia: yeye anayeniamini atafanya vilevile matendo ninayofanya. Na zaidi ya ile atafanya matendo makubwa kuliko haya, kwa sababu ninakwenda kwa Baba. Nami nitafanya chochote mutakachoomba kwa jina langu, kusudi Baba atukuzwe kwa njia ya Mwana. Kama mukiomba kitu chochote kwa jina langu, nitakifanya. “Kama munanipenda, mutashika amri zangu. Nami nitamwomba Baba awape musaidizi mwingine kwa kukaa nanyi milele; naye ndiye Roho wa ukweli. Dunia haiwezi kumupokea, kwa sababu haimwoni wala haimujui. Lakini munamujua, kwa maana anaishi pamoja nanyi naye anakuwa ndani yenu. “Sitawaacha kama wayatima, nitawarudilia tena. Kunabaki wakati kidogo, dunia haitaniona tena, lakini ninyi mutaniona; na kwa sababu mimi ninaishi, ninyi mutaishi vilevile. Na wakati ule mutafahamu kwamba mimi ni ndani ya Baba yangu, na ninyi ni ndani yangu, na mimi ndani yenu. “Anayekubali amri zangu na kuzitii, ni yeye anayenipenda. Baba yangu atamupenda yule anayenipenda, na mimi nitamupenda vilevile na nitajitambulisha kwake.” Yuda (si yule Yuda Iskariota) akamwuliza: “Bwana, namna gani utajitambulisha mwenyewe kwetu wala si kwa dunia?” Yesu akamujibu: “Anayenipenda, atashika maneno yangu. Baba yangu atamupenda, naye Baba pamoja nami tutaingia ndani yake na kukaa ndani yake. Asiyenipenda hashiki maneno yangu. Na neno munalosikia nikisema halitoki kwangu, lakini linatoka kwa Baba yangu aliyenituma. “Nimewaambia maneno haya kwa maana ningali sasa pamoja nanyi. Lakini Musaidizi, ndiye Roho Mutakatifu, yule Baba atakayemutuma kwa jina langu, atawafundisha maneno yote na kuwakumbusha yote niliyowaambia. “Ninawaachia amani; ninawapa amani yangu. Siwapatii ninyi amani hii kama dunia inavyoitoa. Musifazaike wala musiogope. Mumesikia jinsi nilivyowaambia kwamba ninajiendea, lakini nitawarudilia tena. Kama mungenipenda, mungefurahia kujua kwamba ninakwenda kwa Baba, kwa maana Baba ni mukubwa kuliko mimi. Nimewaambia maneno haya sasa mbele hayajatokea, kusudi wakati yatakapotokea, mupate kuamini. Sitasema nanyi maneno mengi tena, kwa sababu mutawala wa dunia hii anakuja. Yeye hana uwezo juu yangu, lakini sherti dunia ijue kama ninamupenda Baba, nami ninafanya kama alivyoniagiza. “Musimame, tutoke hapa. “Mimi ni muzabibu wa kweli, na Baba yangu ni mulimaji. Yeye anakata kila tawi linalokuwa ndani yangu lisilozaa matunda. Naye anasafisha kila tawi linalozaa matunda, kusudi lizae matunda mengi zaidi. Ninyi mumekwisha kuwa safi kwa kuwa mumeshika maneno niliyowaambia. Mukae ndani yangu, nami nitakaa ndani yenu. Tawi haliwezi kuzaa matunda lisipokaa ndani ya muzabibu. Vilevile ninyi hamuwezi kuzaa matunda musipokaa ndani yangu. “Mimi ni muzabibu, nanyi ni matawi. Anayekaa ndani yangu, na mimi ndani yake anazaa matunda mengi, kwa sababu pasipo mimi hamuwezi kufanya kitu. Kama mutu asipokaa ndani yangu, yeye ni kama tawi linalotupwa na kukauka. Matawi yanayokauka yanakusanywa na kutupwa katika moto nayo yanateketea. Kama mukikaa ndani yangu na maneno yangu yanakaa ndani yenu, mutaomba chochote munachotaka, nanyi mutakipewa. Kama mukizaa matunda mengi, Baba yangu atatukuzwa, na hivi mutakuwa kweli wanafunzi wangu. Kama vile Baba anavyonipenda, mimi ninawapenda ninyi vilevile. Mukae katika upendo huu. Kama mukishika amri zangu, mutakaa katika upendo wangu, kama vile mimi nilivyoshika amri za Baba yangu na kukaa katika upendo wake. “Nimewaambia ninyi maneno haya kusudi mufurahi sawa mimi, na furaha yenu ikuwe kubwa kabisa. Hii ndiyo amri ninayowapa: mupendane ninyi kwa ninyi kama ninavyowapenda. Hakuna anayekuwa na upendo mukubwa kuliko mutu anayetoa maisha yake kwa ajili ya warafiki zake. Ninyi ni warafiki zangu, kama mukifanya sawa ninavyowaagiza. Siwaiti ninyi tena watumishi, kwa sababu mutumishi hajui mambo bwana wake anayofanya. Ninawaita ninyi warafiki kwa sababu nimewajulisha yote niliyosikia kutoka kwa Baba yangu. Ninyi hamukunichagua mimi, lakini ni mimi niliyewachagua ninyi. Nami nimewatuma muende kuzaa matunda yasiyokuwa na mwisho. Kwa hiyo Baba atawapa chochote munachoomba kwa jina langu. Amri ninawapa ni kwamba mupendane ninyi kwa ninyi. “Kama dunia ikiwachukia ninyi, mujue kwamba ilinichukia mimi mbele ya kuwachukia. Kama mungekuwa watu wa dunia, dunia ingewapenda, kwa maana ninyi ni watu wake. Lakini nimewachagua ninyi toka dunia hii, na ninyi si watu wa dunia tena. Ni kwa sababu hii dunia inawachukia. Mukumbuke maneno niliyowaambia kwamba mutumishi si mukubwa kuliko bwana wake. Kama walinitesa mimi, watawatesa ninyi vilevile. Na kama walishika maneno yangu, watashika maneno yenu vilevile. Lakini watawafanyia ninyi haya yote kwa ajili yangu, kwa sababu hawamujui yule aliyenituma. Kama singekuja kusema nao, wasingekuwa na zambi; lakini sasa hawataweza kukana zambi yao. Anayenichukia mimi anamuchukia Baba yangu vilevile. Kama nisingetenda kati yao matendo yasiyofanywa na mutu mwingine, wasingekuwa na zambi. Lakini sasa wameyaona lakini hata hivi wananichukia mimi pamoja na Baba yangu. Lakini wamefanya hivi kusudi maneno haya yaliyoandikwa katika Sheria yao yatimie: ‘Wamenichukia pasipo sababu.’ “Wakati Musaidizi nitakayewatumia toka kwa Baba atakapokuja, atanishuhudia mimi. Yeye ni Roho wa ukweli, naye anakuja toka kwa Baba. Na ninyi vilevile mutanishuhudia, kwa sababu mumekuwa pamoja nami tangu mwanzo. “Nimewaambia maneno hayo, kusudi musikwazwe katika imani yenu. Watawatenga musiingie katika nyumba za kuabudia. Na kutakuwa wakati ambapo wote watakaowaua watazani kwamba wanamutumikia Mungu. Watafanya hivi kwa sababu hawakumujua Baba wala mimi. Lakini ninawaambia maneno haya kusudi wakati ule utakapotimia mupate kukumbuka kwamba nimekwisha kuwaambia. “Sikuwaambia ninyi maneno hayo mbele kwa sababu nilikuwa ningali pamoja nanyi. Sasa ninarudi kwake yule aliyenituma na hakuna mumoja wenu anayeniuliza kwamba ninaenda wapi. Lakini kwa sababu nimewaambia maneno haya, mumesikitika sana. Lakini mimi ninawaambia ukweli: ni faida kwenu mimi niende, kwa maana nisipokwenda, Musaidizi hatakuja kwenu. Lakini nikienda, nitamutuma kwenu. Naye atakapokuja, atahakikisha watu wa dunia hii juu ya zambi zao, juu ya haki yangu, na juu ya hukumu ya Mungu. Kuelekea zambi ni kwa sababu hawaniamini mimi. Kuelekea haki ni kwa sababu ninakwenda kwa Baba, nanyi hamutaniona tena. Na kuelekea hukumu ni kwa sababu mutawala wa dunia hii amekwisha kuhukumiwa. “Ningali na maneno mengi ya kuwaambia, lakini sasa hamujakuwa na uwezo wa kuyafahamu. Lakini wakati yule Roho wa ukweli atakapokuja, atawaongoza ninyi kufuata ukweli wote kabisa. Yeye hatasema kwa mamlaka yake mwenyewe, lakini atasema tu yale atakayosikia, naye atawatangazia ninyi habari za mambo yatakayokuja. Yeye atanitukuza mimi kwa sababu maneno atakayowaambia yatatokana na yale yanayokuwa ndani yangu. Yote Baba anayokuwa nayo ni yangu. Ni kwa sababu hii nilisema kwamba maneno Roho atakayowaambia yatatokana na yale yanayokuwa ndani yangu. “Kunabaki wakati kidogo, ninyi hamutaniona; lakini kisha wakati kidogo mutaniona tena.” Basi wanafunzi wake wamoja wakasemezana hivi: “Yeye anatuambia kwamba kunabakia wakati kidogo nasi hatutamwona, lakini kisha wakati kidogo tutamwona tena. Vilevile anasema kwamba ni kwa sababu anakwenda kwa Baba yake. Maana ya maneno haya yote ni nini?” Nao wakaendelea kuulizana: “Maana ya ‘wakati kidogo’ ni nini? Hatufahamu nini anayosema.” Yesu alitambua kwamba walitaka kumwuliza. Basi akawaambia: “Munaulizana juu ya maneno niliyosema kwamba kunabaki wakati kidogo nanyi hamutaniona, lakini kisha wakati kidogo mutaniona tena? Kweli, kweli ninawaambia: mutalia na kusikitika, lakini watu wa dunia watafurahi. Mutahuzunika, lakini huzuni yenu itageuka kuwa furaha. Wakati mwanamuke anapozaa, anasikia uchungu kwa sababu wakati wake wa kuzaa umetimia. Lakini anapokwisha kuzaa, hakumbuki tena maumivu, kwa sababu ya furaha ya kuzaliwa kwa mutoto. Na sasa ninyi vilevile munasikia uchungu, lakini nitawaona tena, nanyi mutafurahi, wala hakuna mutu atakayeweza kuwahuzunisha tena. “Siku ile itakapotimia, ninyi hamutaniuliza juu ya kitu fulani. Kweli, kweli ninawaambia: Baba atawapa chochote mutakachomwomba kwa jina langu. Mpaka sasa hamujaomba kitu kwa jina langu. Muombe, nanyi mutapewa, na furaha yenu itakuwa kubwa kabisa. “Nimewaambia ninyi maneno hayo kwa mifano. Lakini kutakuwa wakati sitasema nanyi tena kwa mifano, lakini nitawaambia ninyi waziwazi juu ya Baba. Siku ile itakapotimia, mutamwomba Baba kwa jina langu. Mimi sisemi kwamba nitawaombea ninyi kwa Baba, kwa maana Baba mwenyewe anawapenda. Anawapenda ninyi kwa sababu mumenipenda na kuamini kwamba nilitoka kwa Mungu. Nilitoka kwa Baba, nami nimekuja katika dunia. Sasa ninaacha dunia na kurudi kwa Baba.” Basi wanafunzi wake wakamwambia: “Sasa unasema waziwazi pasipo kutumia mifano. Sasa tunajua kwamba unajua yote na si lazima mutu akuulize kitu. Sababu hii tunaamini kama ulitoka kwa Mungu.” Yesu akawauliza: “Munaamini sasa? Kutakuwa wakati, nao umetimia, ndio wakati mutakaposambazwa, kila mutu akijiendea ngambo yake mwenyewe, nanyi mutaniacha peke yangu. Lakini mimi si peke yangu kabisa, kwa sababu Baba yuko pamoja nami. Nimewaambia maneno haya kusudi mukuwe na amani, mukibaki katika umoja nami. Mutapata mateso katika dunia. Lakini mujipe moyo, kwa kuwa mimi nimepata ushindi juu ya vyote katika dunia.” Wakati Yesu alipokwisha kusema maneno hayo, akainua macho mbinguni na kusema: “Baba, wakati umetimia. Uonyeshe utukufu wa Mwana wako, kusudi Mwana wako aonyeshe utukufu wako vilevile. Kwa maana ulimupa mamlaka juu ya watu wote, kusudi awapatie uzima wa milele wale wote uliomupa. Nao uzima wa milele ni kukujua wewe unayekuwa peke yako Mungu wa kweli na Yesu Kristo uliyemutuma. Mimi nimekutukuza wewe katika dunia kwa kuwa nimemaliza kazi ile uliyonipa. Na sasa, Baba, unipe utukufu karibu nawe, utukufu unaokuwa sawa na ule niliokuwa nao pamoja nawe mbele ya kuumbwa kwa dunia. “Nimekujulisha kwa watu wale ulionipa, ukiwachagua katika dunia. Wao walikuwa watu wako, uliwatoa kwangu, nao walishika neno lako. Sasa wanajua kwamba yote uliyonipa yanatoka kwako; kwa maana nimewatangazia maneno yale uliyoniagiza, nao wameyakubali. Wamejua hakika kwamba nilitoka kwako na kuamini kwamba wewe ndiwe uliyenituma. “Ninawaombea wao; siwaombei watu wa dunia, lakini hao ulionipa, kwa sababu wao ni wako. Na yote ninayokuwa nayo ni yako, na yote unayokuwa nayo ni yangu, nami nimetukuzwa kwa njia yao. Mimi sitabaki tena katika dunia, lakini wao wangali katika dunia na mimi ninakuja kwako. Baba Mutakatifu, uwalinde kwa uwezo wa jina lako, lile jina ulilonipa, kusudi wakuwe mumoja kama vile sisi tunavyokuwa mumoja. Wakati nilipokuwa pamoja nao, niliwalinda kwa uwezo wa jina lako, ndilo lile jina ulilonipa. Nimewachunga wala hakuna mumoja wao aliyepotea, isipokuwa yule anayepaswa kupotea, kusudi Maandiko Matakatifu yatimizwe. Lakini sasa ninarudi kwako, nami ninasema maneno haya nikingali katika dunia, kusudi furaha yangu kubwa kabisa ikuwe ndani yao. Mimi nimetangaza neno lako kwao, na dunia imewachukia kwa sababu wao si wa dunia, kama vile mimi nisivyokuwa wa dunia. Sikuombi kama uwaondoe katika dunia, lakini ninakuomba uwakinge na yule Mwovu Shetani. Wao si wa dunia, kama vile mimi nisivyokuwa wa dunia. Uwatakase wapate kujitoa kwako kabisa kwa njia ya ukweli, maana yake kwa njia ya neno lako la kweli. Kama vile ulivyonituma katika dunia, mimi vilevile nimewatuma katika dunia. Ninajitoa kwako kabisa mimi mwenyewe kwa ajili yao, kusudi wao vilevile wapate kujitoa kwako kabisa. “Siwaombei hawa tu, lakini ninawaombea vilevile wale watakaoamini kwa sababu ya mafundisho yao. Ninaomba kusudi wote wakuwe mumoja, kama vile wewe Baba unavyokuwa ndani yangu na mimi ndani yako. Ninaomba vilevile kwamba wakuwe ndani yetu, kusudi dunia ipate kuamini kwamba umenituma. Nami nimewapa utukufu ulionipa, kusudi wakuwe mumoja kama vile sisi tunavyokuwa mumoja. Ninaomba nikuwe ndani yao na wewe ndani yangu, kusudi wapate kuwa mumoja kabisa; na dunia ijue kama wewe ndiwe uliyenituma na kwamba unawapenda kama vile unavyonipenda. “Baba, ninataka wale ulionipa wakuwe pamoja nami pahali nitakapokuwa, nao waone utukufu wangu, ndio ule utukufu ulionipa kwa sababu ulinipenda mbele ya kuumbwa kwa dunia. Baba mwenye haki, ijapokuwa dunia haikujui, mimi ninakujua na hawa wanajua kwamba ulinituma. Nimekujulisha kwao, na nitaendelea kukujulisha kusudi upendo ule unaokuwa nao kwangu ukuwe ndani yao, nami mwenyewe nikuwe ndani yao.” Wakati Yesu alipokwisha kusema maneno hayo, akaondoka pamoja na wanafunzi wake na kuvuka ngambo ya kijito cha Kidroni. Nao wote wakaingia katika bustani iliyokuwa kule. Yuda, yule aliyekuwa amemutoa, alijua pahali pale, kwa sababu Yesu alikuwa akikutana kule mara nyingi pamoja na wanafunzi wake. Yuda akatwaa kundi la waaskari pamoja na walinzi waliotumwa na wakubwa wa makuhani na Wafarisayo. Akakuja nao kwenye bustani wakibeba taa, mienge na silaha. Basi Yesu akiwa mwenye kujua maneno yote yatakayomupata, akawaendea na kuwauliza: “Munamutafuta nani?” Wakamujibu: “Yesu wa Nazareti.” Yesu akawaambia: “Ni mimi.” Na Yuda, yule aliyekuwa amemutoa, alikuwa akisimama pale pamoja nao. Yesu alipowaambia: “Ni mimi,” wakarudi nyuma na kuanguka. Yesu akawauliza tena: “Munamutafuta nani?” Nao wakasema: “Yesu wa Nazareti.” Yesu akajibu: “Nimekwisha kuwaambia kwamba ni mimi. Basi ikiwa ni mimi munayemutafuta, muwaache hawa wanaokuwa nami wajiendee.” Alisema vile kusudi maneno haya aliyosema yapate kutimia: “Sikupoteza hata mumoja kati ya wale ulionipa.” Simoni Petro alikuwa na upanga, akauchomoa na kumukata mutumishi wa Kuhani Mukubwa sikio la kuume. (Jina la mutumishi yule lilikuwa Malko.) Lakini Yesu akamwambia Petro: “Rudisha upanga wako katika kifuko chake! Inanipasa kunywa kikombe cha mateso Baba yangu alichonitayarishia.” Basi lile kundi la waaskari na mukubwa wao pamoja na wale walinzi wa wakubwa wa Wayuda wakamukamata Yesu na kumufunga. Wakamupeleka kwanza kwa Anasi. Anasi alikuwa mukwe wa Kayafa, aliyekuwa Kuhani Mukubwa mwaka ule. Ni Kayafa aliyewashauria Wayuda kwamba ni afazali mutu mumoja akufe kwa ajili ya watu wote. Simoni Petro na mwanafunzi mwingine walimufuata Yesu. Yule mwanafunzi alikuwa akijulikana na Kuhani Mukubwa, kwa hiyo akaingia pamoja na Yesu ndani ya upango wa nyumba ya Kuhani Mukubwa. Lakini Petro alisimama inje karibu na mulango. Yule mwanafunzi mwingine, aliyejulikana na Kuhani Mukubwa, akatoka inje, akasema na mwanamuke aliyelinda mulango, naye akamwachilia Petro kuingia ndani. Yule mwanamuke akamwambia Petro: “Wewe vilevile si mumoja wa wanafunzi wa mutu huyu?” Petro akamujibu: “Hapana! Mimi si mwanafunzi wake.” Watumishi na walinzi walikuwa wamekonga moto kwa sababu wakati ule ulikuwa wa baridi, nao walisimama pale wakiota moto. Petro alisimama pale vilevile, akiota moto pamoja nao. Kuhani Mukubwa akamwuliza Yesu juu ya wanafunzi wake na juu ya mafundisho yake. Yesu akamujibu: “Nilisema na watu wote waziwazi, nilifundisha siku zote katika nyumba za kuabudia na katika hekalu, pahali Wayuda wote wanapokutana. Sikusema kitu kwa uficho. Basi kwa sababu gani unaniuliza mimi? Uwaulize wale waliosikia mambo niliyosema, kwa maana wanajua vizuri nini niliyosema.” Yesu aliposema maneno haya, mumoja wa walinzi waliokuwa karibu naye, akamupiga kofi, akisema: “Ni hivi unavyopaswa kumujibu Kuhani Mukubwa?” Yesu akamujibu: “Kama nimesema vibaya, onyesha ubaya ule. Lakini kama nimesema vizuri, kwa nini unanipiga?” Kisha Anasi akamutuma Yesu, akiwa amefungwa, kwa Kayafa Kuhani Mukubwa. Wakati ule Simoni Petro alikuwa angali pale akiota moto. Basi wakamwuliza: “Wewe vilevile si mumoja wa wanafunzi wa mutu huyu?” Petro akakana, akisema: “Hapana! Mimi si mwanafunzi wake.” Mutumishi mumoja wa Kuhani Mukubwa, aliyekuwa ndugu ya mutu yule Petro aliyemukata sikio, akamwambia: “Mimi sikukuona kule katika bustani pamoja naye?” Lakini Petro akakana tena, na pale pale jogoo akawika. Na kulipokucha asubui mapema, wakamutosha Yesu kwa Kayafa na kumupeleka kwenye nyumba ya liwali. Lakini Wayuda wenyewe hawakuingia ndani ya nyumba ya liwali, kwa maana kwa njia ile wangejichafua na kutoweza kuwa tayari kula karamu ya Pasaka. Kwa hiyo Pilato akawakuta inje, na kuwauliza: “Munamushitaki mutu huyu juu ya nini?” Nao wakamujibu: “Kama asingekuwa mutenda maovu, tusingemuleta kwako.” Pilato akawaambia: “Ninyi wenyewe mumukamate na mumuhukumu kufuatana na sheria yenu.” Wakamujibu: “Sisi hatuna ruhusa ya kuua mutu.” (Ilifanyika hivi kusudi litimie lile neno Yesu alilosema kwa kuonyesha kifo gani atakachokufa.) Halafu Pilato akarudi ndani ya nyumba, akamwita Yesu na kumwuliza: “Wewe ni mufalme wa Wayuda?” Yesu akajibu: “Unasema hivi kutokana na mawazo yako mwenyewe au watu wengine wamekuambia habari zangu?” Pilato akajibu: “Mimi si Muyuda. Watu wa taifa lako na wakubwa wa makuhani ndio waliokuleta kwangu. Umefanya nini?” Yesu akajibu: “Ufalme wangu si wa dunia hii. Ufalme wangu ungekuwa wa dunia hii, watumishi wangu wangenipigania kusudi nisitolewe kwa Wayuda. Lakini sasa ufalme wangu si wa hapa katika dunia.” Halafu Pilato akamwuliza: “Ni kusema wewe ni mufalme?” Yesu akamujibu: “Wewe umesema kwamba mimi ni mufalme. Mimi nimezaliwa na kuja katika dunia kusudi nishuhudie ukweli. Wote wanaokuwa upande wa ukweli, wananisikiliza mimi.” Pilato akamwuliza: “Ukweli ni nini?” Pilato alipokwisha kusema neno hili, akatoka tena inje na kuwaambia Wayuda: “Mimi sioni hata sababu moja ya kumuhukumu mutu huyu. Lakini kufuatana na desturi yenu, ninazoea kuwafungulia mufungwa mumoja wakati wa sikukuu ya Pasaka. Basi munataka niwafungulie mufalme wa Wayuda?” Halafu wakalalamika kwa nguvu: “Hatutaki mutu huyu! Tunataka utufungulie Baraba!” (Yule Baraba alikuwa munyanganyi.) Halafu Pilato akaamuru wamukamate Yesu na kumupiga fimbo. Kisha kwa kumuchekelea, waaskari wakasokota taji na tawi lenye miiba na kumuvalisha nalo juu ya kichwa; vilevile wakamuvalisha nguo nyekundu-nyeusi. Wakafika kila wakati mbele yake na kusema: “Jambo, Mufalme wa Wayuda.” Nao wakamupiga makofi. Pilato akatoka tena inje na kuwaambia Wayuda: “Angalia, nitawaletea naye hapa inje kusudi mupate kujua kwamba mimi sioni hata sababu moja ya kumuhukumu.” Basi Yesu akatoka inje, akivaa ile taji ya miiba na ile nguo nyekundu. Pilato akawaambia watu: “Mutu wenu huyu!” Basi wakati wale wakubwa wa makuhani na walinzi walipomwona, wakapiga kelele, wakisema: “Umutundike juu ya musalaba! Umutundike juu ya musalaba!” Pilato akawaambia: “Mumutwae ninyi wenyewe na kumutundika, kwa maana mimi sioni sababu ya kumuhukumu.” Wayuda wakamujibu: “Kufuatana na moja ya sheria zetu, mutu huyu anapaswa kuuawa, kwa sababu alijiita Mwana wa Mungu.” Pilato aliposikia neno hili, akazidi kuogopa. Akaingia tena katika nyumba yake na kumwuliza Yesu: “Wewe ni muzaliwa wa wapi?” Lakini Yesu hakumujibu neno. Basi Pilato akamwambia: “Hautaki kusema nami? Wewe haujui kama mimi nina mamlaka ya kukufungua na mamlaka ya kukutundika juu ya musalaba?” Yesu akamujibu: “Wewe hauna mamlaka yoyote juu yangu, isipokuwa tu yale uliyopewa na Mungu toka juu. Ni kwa hiyo, yule aliyenitoa kwako anabeba zambi kubwa zaidi.” Tokea saa ile Pilato alitafuta njia ya kumufungua Yesu. Lakini Wayuda wakapiga kelele, wakisema: “Ukimufungua mutu huyu, wewe si rafiki wa Mufalme wa Roma. Kila mutu anayejifanya kuwa mufalme, anamupinga Mufalme wa Roma!” Pilato aliposikia maneno haya, akamupeleka Yesu inje; akaikaa katika kiti cha hukumu kwenye nafasi inayoitwa katika Kiebrania “Gabata,” maana yake “Sakafu ya Mawe.” Siku ile ilikuwa siku ya matayarisho ya Pasaka, karibu na saa sita. Pilato akawaambia Wayuda: “Mufalme wenu huyu!” Lakini wakapiga kelele wakisema: “Umwue! Umwue! Umutundike juu ya musalaba!” Pilato akawauliza: “Munataka nimutundike mufalme wenu juu ya musalaba?” Wakubwa wa makuhani wakajibu: “Sisi hatuna mufalme mwingine isipokuwa Mufalme wa Roma.” Halafu Pilato akamutoa Yesu kwao, kusudi atundikwe juu ya musalaba. Basi wakamukamata Yesu. Yesu akaondoka katika muji akibeba musalaba wake mpaka kwenye nafasi inayoitwa katika Kiebrania “Golgota”, maana yake: “Kilima cha Mufupa wa Kichwa.” Waaskari wakamutundika Yesu juu ya musalaba kule pamoja na watu wengine wawili, mumoja kila upande na Yesu katikati. Pilato akaamuru andiko liandikwe na kuwekwa juu ya musalaba. Nalo liliandikwa hivi: “Yesu wa Nazareti, Mufalme wa Wayuda.” Pahali pale Yesu alipotundikwa palikuwa karibu na muji, kwa hiyo Wayuda wengi walisoma andiko lile. Nalo lilikuwa limeandikwa katika Kiebrania, Kilatini na Kigriki. Basi wakubwa wa makuhani wa Wayuda wakamwambia Pilato: “Usiandike: ‘Mufalme wa Wayuda,’ lakini uandike hivi: ‘Mutu huyu alisema, Mimi ni Mufalme wa Wayuda!’ ” Pilato akajibu: “Yale niliyoandika, yameandikwa!” Waaskari walipokwisha kumutundika Yesu juu ya musalaba wakakamata nguo zake na kuzigawanya katika sehemu ine, wakimupa kila askari sehemu moja. Wakakamata vilevile kanzu yake iliyokuwa bila mushono, iliyofumwa kwa kipande kimoja tu tokea juu mpaka chini. Waaskari wakaambiana: “Tusipasue kanzu hii, lakini tuipigie kura, kusudi tujue itakuwa ya nani.” Mambo haya yalifanyika kusudi Maandiko Matakatifu yanayosema hivi yatimie: “Waligawanya nguo zangu nayo kanzu yangu wakaipigia kura.” Mambo hayo ndiyo waaskari waliyofanya. Mama ya Yesu, dada ya mama yake, Maria muke wa Kleopa na Maria wa muji wa Magdala walikuwa wamesimama karibu na musalaba wake. Basi wakati Yesu alipoona mama yake pale na yule mwanafunzi aliyemupenda, akisimama karibu, akamwambia mama yake: “Mama, sasa huyu ndiye mwana wako.” Na kisha akamwambia yule mwanafunzi: “Sasa huyu ndiye mama yako.” Na tokea saa ile, mwanafunzi yule alimupeleka Maria kwake. Kisha, Yesu akiwa anajua kwamba mambo yote yametimia, akasema hivi kusudi Maandiko Matakatifu yatimie: “Ninasikia kiu.” Pale kulikuwa chombo chenye kujaa divai yenye kuchacha. Basi waaskari wakachovya kikausho ndani ya ile divai, wakakifungia juu ya tawi la hisopo na kukiweka kwa kinywa chake. Wakati Yesu alipokwisha kumeza ile divai, akasema: “Yote yametimilika!” Kisha akainamisha kichwa na kukata roho. Siku ile ilikuwa ya matayarisho ya siku ya Sabato iliyofuata. Kwa sababu hii Wayuda hawakutaka maiti za wale waliotundikwa zibaki juu ya misalaba kwa maana siku ile ilikuwa kubwa sana. Kwa hiyo wakamwomba Pilato ruhusa kwamba miguu ya wale waliotundikwa ivunjwe kusudi wakufe mbio na maiti zao ziondoshwe. Basi waaskari walikuja, wakavunja miguu ya mutu wa kwanza na kisha miguu ya yule wa pili aliyetundikwa pamoja na Yesu juu ya musalaba. Lakini walipofika kwenye Yesu, walikuta amekwisha kufa; kwa hiyo hawakumuvunja miguu. Lakini askari mumoja akamuchoma mukuki katika ubavu; mara moja damu na maji vikatoka. Mutu aliyeona mambo hayo ndiye anayeyashuhudia, nao ushuhuda wake ni wa kweli. Na anajua kama anasema ukweli, kusudi mupate kuamini vilevile. Mambo haya yalifanyika kusudi Maandiko Matakatifu yanayosema hivi yatimie: “Hakuna hata mufupa wake mumoja utakaovunjwa.” Na tena Maandiko mengine Matakatifu yanasema: “Watamwangalia yule waliyemutoboa kwa mukuki.” Nyuma ya mambo hayo, Yosefu, mutu wa Arimatea, akamwomba Pilato ruhusa ya kuondoa maiti ya Yesu. (Yosefu alikuwa mumoja wa wanafunzi wa Yesu lakini kwa siri, kwa sababu aliwaogopa wakubwa wa Wayuda.) Pilato akamuruhusu. Basi Yosefu akaenda na kuondoa maiti ya Yesu. Naye Nikodemo, yule aliyemwendea Yesu siku moja usiku, alikuja vilevile. Alikuwa akileta yapata kilo makumi tatu ya marasi yaliyochangwa na udi. Wote wawili wakatwaa maiti ya Yesu, wakaifunga na vitambaa vyenye kupakaliwa mafuta zenye harufu nzuri sawa na desturi za maziko za Wayuda. Kulikuwa bustani pale walipomutundika Yesu, na katika bustani ile kulikuwa kaburi jipya, mulimokuwa hamujazikwa mutu. Na kwa kuona siku ile ilikuwa ya matayarisho ya siku ya Sabato ya Wayuda na kaburi lilikuwa karibu, wakamuzika Yesu mule. Siku ya kwanza ya juma asubui mapema, kulipokuwa kungali giza, Maria wa Magdala akaenda kwenye kaburi. Alipofika kule akaona kama jiwe lililofunika kaburi limeondolewa. Basi akaenda mbio kwa Simoni Petro na kwa yule mwanafunzi mwingine aliyependwa na Yesu na kuwaambia: “Wameondoa maiti ya Bwana toka katika kaburi na hatujui pahali walipoiweka.” Basi Petro na yule mwanafunzi mwingine wakaondoka na kwenda kwenye kaburi. Wakaenda mbio wakikimbia wote wawili pamoja, lakini yule mwanafunzi alikimbia mbio zaidi kuliko Petro, akamutangulia kwenye kaburi. Yeye akainama na kuchungulia ndani yake, akaona vitambaa vimewekwa pembeni, lakini hakuingia. Kisha Simoni Petro akafika nyuma yake na kuingia ndani ya kaburi. Akaona vitambaa vimewekwa pembeni, vilevile akaona kitambaa kilichofunika kichwa cha Yesu. Kitambaa kile hakikuwekwa pamoja na vile vingine, lakini kilikuwa kimekunjwa na kuwekwa peke yake pahali pengine. Halafu yule mwanafunzi mwingine aliyetangulia kwenye kaburi akaingia vilevile. Akapata kujionea na kuamini. (Ilikuwa vile kwa maana wanafunzi walikuwa hawajaelewa bado Maandiko Matakatifu yanayosema kwamba Yesu anapaswa kufufuka.) Kisha mambo hayo hawa wanafunzi wawili wakarudi kwao. Maria alikuwa akisimama inje karibu na kaburi, akilia. Alipokuwa akilia, akainama na kuangalia ndani ya kaburi, akaona wamalaika wawili wanaovaa nguo nyeupe wakiikaa pahali maiti ya Yesu ilipowekwa. Mumoja alikuwa kwa upande wa kichwa na mwingine upande wa miguu. Wale wamalaika wakamwuliza: “Ee mama, kwa sababu gani unalia?” Naye akawajibu: “Kwa sababu wameondoa maiti ya Bwana, nami sijui pahali walipoiweka.” Alipokwisha kusema maneno haya, akageuka nyuma, akamwona Yesu akisimama pale, lakini hakutambua kwamba ni yeye. Yesu akamwuliza: “Mama, kwa sababu gani unalia? Unamutafuta nani?” Maria akizani kwamba ni mulimaji wa bustani, akamwambia: “Bwana, kama ni wewe uliyeondoa maiti yake, uniambie pahali ulipoiweka, nami nitakwenda kuitwaa.” Yesu akamwambia: “Maria!” Naye akageuka, akasema kwa kiebrania: “Raboni,” maana yake “Mwalimu.” Yesu akamwambia: “Usinishike, kwa sababu sijapanda bado kwa Baba. Lakini kwenda kwa wandugu zangu na kuwaambia kwamba ninapanda kwa Baba yangu anayekuwa Baba yenu vilevile, anayekuwa Mungu wangu na Mungu wenu vilevile.” Basi Maria wa Magdala akaenda kuwapasha wanafunzi habari kama amemwona Bwana, na kwamba amemwambia maneno hayo. Magaribi ya ile ile siku ya kwanza ya juma, wanafunzi walikusanyika katika nyumba na milango ilikuwa imefungwa, kwa sababu waliwaogopa wakubwa wa Wayuda. Mara moja Yesu akawatokea na kusimama katikati yao, akawaambia: “Amani kwenu!” Kisha kusema hivi, Yesu akawaonyesha mikono yake na ubavu wake. Basi wanafunzi wakafurahi wakati walipomwona Bwana. Yesu akawaambia tena: “Amani kwenu! Kama vile Baba alivyonituma, mimi ninawatuma ninyi vilevile.” Alipokwisha kusema maneno haya, akawapulizia pumzi na kuwaambia: “Mupokee Roho Mutakatifu. Watu wote mutakaowasamehe zambi, watasamehewa; nao wote musiowasamehe, hawatasamehewa.” Lakini Toma, anayeitwa “Pacha,” aliyekuwa mumoja wa wale wanafunzi kumi na wawili, hakukuwa pamoja nao wakati Yesu alipokuja. Wanafunzi wengine wakamwambia: “Tumemwona Bwana.” Lakini Toma akawajibu: “Nisipoona alama za misumari katika mikono yake na kutia kidole changu katika kovu za misumari ile, nami nisipoingiza vidole vyangu ndani ya ubavu wake, sitaamini.” Ilipotimia juma moja nyuma ya pale, wanafunzi wa Yesu wakakusanyika tena ndani ya nyumba ile ile, na mara hii Toma alikuwa pamoja nao. Ijapokuwa milango ilikuwa imefungwa, Yesu akawatokea tena, akasimama katikati yao na kusema: “Amani kwenu!” Kisha akamwambia Toma: “Ujongeze kidole chako hapa na uione mikono yangu; unyooshe mukono wako na kugusa ndani ya ubavu wangu. Usikuwe tena na mashaka, lakini uamini.” Toma akamujibu: “Bwana wangu na Mungu wangu!” Na Yesu akamwambia: “Umeamini kwa sababu umeniona? Heri wale wanaoamini pasipo kuona!” Yesu alionyesha vitambulisho vingine vingi mbele ya wanafunzi wake visivyoandikwa katika kitabu hiki. Lakini hii imeandikwa kusudi mupate kuamini kwamba Yesu ni Kristo, Mwana wa Mungu, na kwa kumwamini mupate uzima katika jina lake. Nyuma ya mambo hayo, Yesu akawatokea tena wanafunzi wake kandokando ya ziwa la Tiberia. Angalia sasa namna alivyowatokea: Simoni Petro, Toma (anayeitwa Pacha), Natanaeli (wa muji Kana katika Galilaya), nao wana wa Zebedayo pamoja na wanafunzi wengine wawili wa Yesu, wote walikuwa pamoja. Simoni Petro akawaambia wenzake hivi: “Ninakwenda kuvua samaki.” Nao wakamwambia: “Na sisi vilevile tutakwenda pamoja nawe.” Basi wakaondoka, wakaingia katika chombo. Usiku ule hawakupata kitu. Asubui mapema, Yesu akaonekana kandokando ya ziwa, lakini wanafunzi hawakutambua kwamba ni yeye. Basi Yesu akawauliza: “Watoto wangu, mumepata samaki?” Wakamujibu: “Hapana.” Yeye akawaambia: “Mutupe wavu upande wa kuume wa chombo na mutapata samaki.” Basi wakatupa wavu, nao wakashindwa kuukokota, kwa sababu ulikuwa umejaa samaki wengi. Halafu mwanafunzi yule aliyependwa na Yesu akamwambia Petro: “Ni Bwana.” Simoni Petro aliposikia kwamba ni Bwana, akavaa kanzu yake (kwa maana alikuwa havai kitu), naye akajitupa ndani ya maji. Wanafunzi wengine wakakuja katika chombo wakikokota wavu uliojaa samaki. Nao hawakukuwa mbali kabisa na inchi kavu, iliwabakilia yapata metre mia moja tu. Walipofika inchi kavu wakaona mukate na samaki zinazokuwa juu ya moto. Yesu akawaambia: “Mulete sehemu ya samaki munaotoka kuvua.” Basi Simoni Petro akapanda ndani ya chombo, akakokota wavu mpaka inchi kavu. Nao ulikuwa umejaa samaki wakubwa mia moja makumi tano na tatu. Na ijapokuwa walikuwa wengi vile, wavu haukupasuka. Yesu akawaambia: “Mukuje mukule.” Na hakuna hata mumoja kati ya wanafunzi aliyesubutu kumwuliza kwamba yeye ni nani, kwa maana walijua kwamba ni Bwana. Basi Yesu akawajongelea, akatwaa mukate, akawagawanyia; na kuwapa samaki vilevile. Hii ndiyo mara ya tatu Yesu aliyowatokea wanafunzi wake tangu alipofufuka. Walipokwisha kula, Yesu akamwuliza Simoni Petro: “Simoni mwana wa Yoane, unanipenda mimi kuliko hawa?” Naye akamujibu: “Ndiyo, Bwana, unajua kama ninakupenda!” Yesu akamwambia: “Tunza wana-kondoo wangu.” Akamwuliza tena mara ya pili: “Simoni mwana wa Yoane, unanipenda?” Naye akamujibu: “Ndiyo, Bwana, unajua kama ninakupenda!” Yesu akamwambia tena: “Chunga kondoo wangu.” Kisha Yesu akamwuliza mara ya tatu: “Simoni mwana wa Yoane, unanipenda?” Basi Petro akauzika kwa sababu Yesu alimwuliza mara ya tatu kama anamupenda. Kwa hiyo akamujibu: “Bwana, unajua yote; unajua kama ninakupenda!” Yesu akamwambia: “Tunza kondoo wangu. Ninakuambia mambo ya kweli: wakati ulipokuwa kijana, ulijivalisha wewe mwenyewe na kwenda pahali ulipotaka. Lakini wakati utakapokuwa muzee, utanyoosha mikono yako na mutu mwingine atakuvalisha na kukupeleka pahali usipotaka.” (Yesu alisema maneno haya kwa kuonyesha kifo gani Petro atakachokufa na kumutukuza Mungu.) Kisha kusema maneno haya, Yesu akamwambia: “Unifuate!” Petro akageuka, akaona nyuma yao mwanafunzi yule aliyependwa na Yesu. (Ni yeye aliyeegamia kifua cha Yesu wakati wa chakula na kumwuliza: “Bwana, ni nani yule atakayekutoa?”) Basi wakati Petro alipomwona, akamwuliza Yesu: “Bwana, na mutu huyu, ni nini itakayomufikia?” Yesu akamujibu: “Ikiwa ninataka huyu aishi mpaka nitakaporudi, jambo hili halikuangalii! Wewe, unifuate!” Basi habari hii ikaenea kati ya wandugu waamini wa Yesu kwamba yule mwanafunzi hatakufa. Yesu hakusema kama hatakufa; lakini alisema: “Ikiwa ninataka huyu aishi mpaka nitakapokuja, jambo hili halikuangalii.” Ni huyu huyu mwanafunzi ndiye aliyeshuhudia mambo hayo na kuyaandika; nasi tunajua kwamba ushuhuda wake ni wa kweli. Kuna mambo mengine mengi Yesu aliyofanya. Lakini yote yangeandikwa moja kwa moja, ninazani hata dunia nzima haingetosha kwa kuwekea vitabu ambavyo vingeandikwa. Katika kitabu changu cha kwanza nilikuelezea mambo yote Yesu aliyofanya na kufundisha tangu alipoanza kazi yake mpaka siku ile aliponyanyuliwa mbinguni. Mbele ya kunyanyuliwa kule, alitoa maagizo kwa njia ya Roho Mutakatifu kwa watu aliokuwa amewachagua kuwa mitume wake. Nyuma ya kufa kwake, alijionyesha kwao kwa namna nyingi kwa kuhakikisha kwamba amefufuka. Kwa muda wa siku makumi ine, alionekana kwao na kusema nao juu ya maneno yanayoelekea Ufalme wa Mungu. Siku moja alipokuwa akikusanyika pamoja nao, akawaagiza: “Musitoke Yerusalema, lakini mubaki kule mukingojea zawadi ambayo Baba yangu aliahidi, ile niliyowaambia ninyi. Kwa maana Yoane alibatiza kwa maji, lakini kisha siku chache, ninyi mutabatizwa kwa Roho Mutakatifu.” Basi mitume walipokusanyika pamoja na Yesu, wakamwuliza: “Bwana, wakati huu ndio utakapowarudishia Waisraeli ufalme wao?” Yesu akawajibu: “Si kazi yenu kutambua siku wala nyakati Baba yangu alizopanga kwa mamlaka yake mwenyewe. Lakini mutapokea uwezo wakati Roho Mutakatifu atakaposhuka juu yenu. Nanyi mutakuwa washuhuda wangu katika Yerusalema, katika Yudea yote na Samaria na hata katika inchi zote za dunia.” Kisha kusema maneno haya, Yesu akanyanyuliwa mbinguni, nao walikuwa wakimwangalia. Na wingu likamuficha hata hawakumwona tena. Walipokuwa wangali wakiangalia mbinguni wakati Yesu alipopanda, kwa rafla kukaonekana watu wawili wanaovaa nguo nyeupe, wakasimama karibu nao. Watu hao wakawaambia: “Ninyi Wagalilaya, sababu gani munasimama pale mukiangalia mbinguni? Huyu Yesu aliyenyanyuliwa toka katikati yenu kwenda mbinguni, atarudi sawa vile mulivyomwona akienda.” Kisha mitume wakarudi Yerusalema tokea kwenye mulima wa Mizeituni unaokuwa karibu na muji huo kwenye umbali wa yapata kilometre moja. Walipofika katika muji wakapanda katika chumba cha gorofi walipokuwa wanazoea kukutanana. Na waliokuwa pale ni hawa: Petro, Yoane, Yakobo, Andrea, Filipo, Toma, Bartolomayo, Matayo, Yakobo mwana wa Alfayo, Simoni wa kikundi cha Wazeloti na Yuda mwana wa Yakobo. Hawa wote walikuwa wakikusanyika kwa nia moja kwa kuomba, pamoja na wanawake wamoja, Maria mama wa Yesu, na wandugu za Yesu. Katika siku zile, kulikuwa mukutano wa wandugu waamini yapata watu mia moja makumi mbili. Basi Petro akasimama katikati yao, akasema: “Wandugu zangu, ilikuwa lazima yale Maandiko Matakatifu yatimie ambayo Roho Mutakatifu alitabiri kwa kinywa cha mufalme Daudi juu ya Yuda, yule aliyewaongoza wale waliomukamata Yesu. Yuda alikuwa mumoja wa kundi letu, naye alikuwa ameshiriki pamoja nasi katika kazi hii.” (Yuda alinunua shamba kwa njia ya feza alizopata kwa ajili ya kitendo chake cha uovu. Pale akaangukia kichwa chini, maiti yakapasuka na matumbotumbo yake yote yakatoka inje. Jambo hilo likajulikana na wakaaji wote wa Yerusalema, hata wakaita shamba lile katika luga yao “Akeldama,” maana yake, “Shamba la Damu.”) “Kwa sababu imeandikwa hivi katika kitabu cha Zaburi: ‘Makao yake yabakie ukiwa na mutu asiishi ndani yake.’ Na imeandikwa tena: ‘Mutu mwingine atwae kazi yake.’ Basi wakataja watu wawili: mumoja alikuwa Yosefu, aliyeitwa vilevile Barisaba na aliyejulikana vilevile kwa jina la Yusto, na mwingine Matia. Kisha wakaomba wakisema: “Bwana, wewe unayejua yanayokuwa ndani ya mioyo ya watu wote, utuonyeshe ni nani uliyemuchagua kati ya hawa wawili kusudi atiwe katika kazi hii ya kuwa mutume kwenye nafasi Yuda aliyoacha na kwenda pahali pake mwenyewe.” Halafu wakapiga kura, na kura ikamwangukia Matia. Naye akaongezwa katika kundi la wale mitume kumi na mumoja. Wakati siku ya Pentekoste ilipotimia, wanafunzi walikuwa wamekusanyika wote pamoja wakibaki kwenye nafasi moja. Mara moja uvumi uliokuwa kama upepo unaovuma kwa nguvu sana ukashuka kutoka mbinguni. Nao ukajaa ndani ya nyumba yote walimokuwa wakiikaa. Kisha wakaona mufano wa ndimi za moto zikitokea, nazo zikasambaa na kushuka juu ya kila mumoja wao. Wote wakapewa Roho Mutakatifu na kuanza kusema kwa luga mbalimbali kwa kadiri Roho alivyowawezesha kusema. Katika Yerusalema kulikaa Wayuda wamoja waliotoka katika inchi zote za dunia, nao walikuwa watu wenye kuogopa Mungu. Wakati waliposikia ile fujo, wakakusanyika kwa uwingi. Wote wakapigwa na mushangao, kwa sababu kila mumoja wao aliwasikia waamini wakisema katika luga yake ya kuzaliwa. Wakashituka na kushangaa, wakisema: “Hawa wote wanaosema si wazaliwa wa Galilaya? Basi namna gani kila mumoja wetu anawasikia wakisema luga yake ya kuzaliwa? Kati yetu kuna watu wenye kutoka katika inchi hizi: Parti, Medi, Elamu, Mesopotamia, Yudea, Kapadokia, Ponto, Jimbo la Azia, Furigia, Pamfilia, Misri na pande za Libya karibu na Kurene. Vilevile kuna wageni waliotoka Roma, kati yao kuna Wayuda na watu waliofuata dini ya Kiyuda, na kuna watu wa inchi ya Krete na ya Arabia. Hata hivi tunawasikia hawa wote wakisema habari za matendo makubwa ya Mungu katika luga zetu za kuzaliwa!” Wote wakashituka na kushangaa, wakaulizana: “Maana ya mambo haya ni nini?” Lakini wengine waliwachekelea waamini, wakisema: “Watu hawa wamelewa kabisa.” Basi Petro akasimama pamoja na wale mitume wengine kumi na mumoja na kuanza kusema kwa sauti kubwa mbele ya watu: “Ninyi Wayuda, nanyi wote munaokaa Yerusalema, musikilize vizuri, mutege sikio kwa maneno nitakayowaambia. Watu hawa si walevi kama munavyozani, kwa sababu ingali tu saa tatu ya asubui. Lakini jambo hili ni lile lililosemwa na nabii Yoeli. ‘Mungu anasema: Katika siku za mwisho, nitashusha Roho wangu juu ya watu wote; wana wenu na wabinti zenu watatabiri, vijana wenu wataona maono nao wazee wenu wataota ndoto. Hakika katika siku zile nitashusha Roho wangu juu ya watumishi wangu, wanaume na wanawake, nao watatabiri. Nami nitafanya maajabu juu katika mbingu na vitambulisho chini katika dunia: kutakuwa damu, moto na moshi mwingi. Jua litatiwa giza, mwezi utakuwa kama damu, mbele ya kutimia kwa siku ya Bwana, ile siku kubwa na ya utukufu. Halafu watu wote watakaoomba kwa jina la Bwana ataokolewa.’ “Ninyi wanainchi wenzangu Waisraeli, musikilize maneno haya: Yesu wa Nazareti alikuwa mutu aliyetambulishwa wazi na Mungu mbele yenu kwa njia ya vitambulisho, miujiza, na maajabu aliyofanya katikati yenu kama munavyojua ninyi wenyewe. Mutu huyu alitolewa kwenu kufuatana na mupango uliokusudiwa na kujulikana na Mungu tangu zamani. Nanyi mulimwua, kwa kumutia katika mikono ya wenye zambi wamutundike juu ya musalaba. Lakini Mungu alimufufua, akimufungua toka vifungo vya lufu, kwa sababu haikuwezekana afungwe na lufu. Kwa maana mufalme Daudi alisema hivi juu yake: ‘Nilikuwa nikimwona Bwana mbele yangu saa zote; yeye ni karibu nami, kusudi nisitikisike. Ni kwa hiyo moyo wangu unafurahi, ulimi wangu unashangilia, nami ninakaa na matumaini, maana hautaniachilia kubaki katika kuzimu, hautakubali mutumishi wako mutakatifu apate kuoza. Umenionyesha njia za uzima, utanijaza furaha nitakapokuwa karibu nawe.’ “Wandugu, inanipasa kuwaambia kwa uhodari juu ya babu yetu mukubwa Daudi. Yeye alikufa na kuzikwa, nalo kaburi lake lingali hata leo. Lakini kwa sababu alikuwa nabii, alijua kwamba Mungu amemwahidi kwa kiapo kwamba atamutawalisha mumoja wa wazao wake kwa kurizi ufalme wake. Daudi aliona kwa mbali yale yatakayotokea, ni kwa sababu hii alisema maneno haya juu ya ufufuko wa Kristo: ‘Hakuachiliwa kubaki katika kuzimu, wala mwili wake haukuoza.’ “Mungu alimufufua huyo Yesu, na sisi wote tuko washuhuda wa jambo hili. Na kisha kunyanyuliwa aikae na mamlaka kwa kuume kwa Mungu Baba yake, yeye akamupa Roho Mutakatifu aliyeahidiwa. Naye akamushusha juu yetu, sawa vile munavyojionea na kusikia wenyewe. Maana Daudi mwenyewe hakupanda mbinguni, lakini alisema: ‘Bwana wetu Mungu alimwambia Bwana wangu: Ikaa na mamlaka kwa kuume kwangu, mpaka nitakapowaweka waadui zako chini ya miguu yako, wakuwe kama kiti cha kupumzishia miguu.’ “Kwa hiyo watu wa taifa la Israeli wajue hakika kwamba yule Yesu muliyemutundika juu ya musalaba, Mungu amemufanya kuwa Bwana na Masiya!” Nao watu waliposikia maneno hayo, wakachomwa katika mioyo yao na kuwaambia Petro na mitume wengine: “Wandugu zetu, tufanye nini?” Petro akawajibu: “Mugeuke toka katika zambi zenu, na kila mumoja wenu abatizwe kwa jina la Yesu Kristo, na Mungu atawasamehe zambi zenu. Hivi mutapokea zawadi ya Roho Mutakatifu. Kwa maana ahadi hii ya Mungu ilitolewa kwenu, kwa watoto wenu na kwa wote wanaokaa mbali, ndio wote ambao Bwana Mungu wetu atakaowaita.” Petro akazidi kusema maneno mengine ya kuwaonya na kuwatia moyo, akisema: “Mujiokoe toka kati ya kizazi hiki kipotovu!” Siku ile watu waliosadiki mafundisho ya Petro, wakabatizwa. Na kadiri ya watu elfu tatu wakaongezeka katika kundi la wanafunzi. Nao walikuwa wakijitoa kufuata mafundisho ya mitume, kuishi katika ushirika wa kindugu, kumega mukate na kuomba. Kila mumoja wao akaingiwa na woga, nao mitume walifanya maajabu na vitambulisho vingi. Na wanafunzi wote waliishi katika umoja na katika ushirika wa vitu vyao vyote. Waliuzisha mali zao na vyote walivyokuwa navyo na kugawanya kati yao kufuatana na mahitaji ya kila mutu. Kila siku walikuwa wakikusanyika pamoja katika hekalu, nao walikula chakula pamoja katika nyumba zao kwa furaha na katika unyenyekevu. Nao walisifu Mungu na kufurahiwa na watu wote. Na kila siku Bwana aliongeza katika kundi la waamini watu waliokuwa wakiokolewa. Siku moja, na saa tisa ya muchana, Petro na Yoane walienda katika hekalu kwa wakati wa maombi. Karibu na mulango mumoja wa hekalu unaoitwa “Muzuri,” kulikuwa mutu mumoja aliyekuwa kiwete tangia kuzaliwa kwake. Kila siku walimubeba na kumuweka kwenye mulango huo kusudi aombe musaada kwa watu waliokuwa wakiingia katika hekalu. Yule kiwete alipowaona Petro na Yoane wakiingia ndani ya hekalu, akawaomba musaada. Petro na Yoane wakamukazia macho, naye Petro akamwambia: “Utuangalie!” Yule kiwete akawaangalia, akitumainia kupata kitu fulani toka kwao. Lakini Petro akamwambia: “Sina mali yoyote, lakini nitakupa kile ninachokuwa nacho. Kwa jina la Yesu Kristo wa Nazareti, ninakuamuru simama utembee!” Halafu Petro akamushika mukono wa kuume na kumusimamisha. Na pale pale miguu na vifundo vya miguu yake vikakaza kwa nguvu; akaruka, akasimama na kuanza kutembea. Kisha akaingia pamoja nao ndani ya hekalu akitembea, akirukaruka na kumusifu Mungu. Watu wote waliokuwa mule walimwona akitembea na kumusifu Mungu. Walipotambua kwamba yeye ndiye yule kiwete aliyekuwa akiikaa na kuombaomba musaada kwenye mulango wa hekalu unaoitwa “Muzuri,” wakashikwa na hofu na kushangaa sana na mambo yale yaliyomutokea. Mutu huyo hakutaka kuachana na Petro na Yoane. Kwa hiyo watu wote wakashangaa sana na kukimbilia kwenye baraza la hekalu wanaloita La Solomono. Petro alipoona maneno yale, akawaambia watu: “Wanainchi wenzangu Waisraeli, sababu gani munashangazwa na jambo hili? Sababu gani munatukazia macho? Munafikiri kwamba mutu huyu amepata kutembea kutokana na uwezo wetu sisi wenyewe au kwa haki yetu mbele ya Mungu? Mungu wa Abrahamu, Isaka na Yakobo, Mungu wa babu zetu, ameonyesha kwamba mutumishi wake Yesu ni mwenye utukufu. Ninyi wenyewe mulimutoa na kumukana mbele ya mutawala Pilato, ijapokuwa Pilato alikuwa ameamua kwamba afunguliwe. Yeye alikuwa Mutakatifu na Mwenye Haki, lakini mukamukana, mukataka Pilato awafungulie mwuaji. Halafu mukamwua yule anayekuwa asili ya uzima, lakini Mungu amemufufua. Na sisi ni washuhuda wa jambo hilo. Mutu huyu munayemujua na kumwona amepata tena nguvu kwa uwezo wa jina la Yesu, kwa njia ya kuaminia jina hili. Yeye amepona kabisa sawa vile ninyi wote munavyojionea, kwa njia ya kumwaminia Yesu. “Sasa wandugu zangu, ninajua kwamba ninyi na wakubwa wenu mumemutendea Yesu hayo yote pasipo kujua nini munayofanya. Lakini ni hivi Mungu alivyotimiza maneno aliyotangaza tangu zamani kwa kinywa cha manabii wote kwamba Masiya wake atateswa. Basi mugeuke toka katika zambi, mumurudilie Mungu, kusudi awasamehe zambi zenu. Hivi Bwana atawaletea nyakati za kutulizwa, naye atawatumia Masiya, ndiye Yesu, aliyechaguliwa tangu zamani kwa kuwaokoa. Yeye anapaswa kubaki mbinguni mpaka zitakapotimia zile nyakati Mungu atakapotengeneza vitu vyote sawa vile alivyosema tangu zamani kwa kinywa cha manabii wake watakatifu. Kwa maana Musa alisema: ‘Bwana Mungu wenu atawatumia ninyi nabii anayekuwa sawa mimi, toka katika taifa lenu. Nanyi mutasikiliza mambo yote nabii yule atakayowaambia. Na mutu yeyote atakayekataa kumusikiliza nabii yule, atatengwa mbali na taifa la Mungu na kuuawa.’ Na manabii waliosema tangia Samweli na wale waliomufuata, wote walitangaza mambo haya yanayotokea siku hizi. Ahadi Mungu alizotoa kwa njia ya manabii ni kwenu. Vilevile agano Mungu alilofanya na babu zenu ni kwa ajili yenu, wakati alipomwambia Abrahamu: ‘Kwa njia ya wazao wako watu wote wa dunia watabarikiwa.’ Hivi Mungu alimutuma mutumishi wake kwa ajili yenu kwanza, kusudi awabariki ninyi, akimugeuza kila mumoja wenu toka katika njia zake mbaya.” Petro na Yoane walipokuwa wangali wakisema mbele ya watu, makuhani, mukubwa wa walinzi wa hekalu pamoja na Wasadukayo wakafika. Wao walichukizwa sana kwa sababu wale mitume wawili walikuwa wakiwafundisha watu na kutangaza kwao kwamba Yesu alifufuka, nao ufufuko wake unahakikisha kwamba wafu watafufuka. Kwa hiyo wakawakamata na kuwatia katika kifungo mpaka kesho yake kwa maana ilikuwa imekwisha kuwa magaribi. Lakini wengi kati ya watu waliosikia mafundisho ya Petro na Yoane wakaamini. Kadiri ya watu elfu tano wakaongezeka katika kundi la waamini. Kesho yake, wasimamizi wa Wayuda, wazee na walimu wa Sheria wakakusanyika Yerusalema. Kulikuwa vilevile Kuhani Mukubwa Anasi, Kayafa, Yoane, Alesanduro na watu wengine wote wa ukoo wa Kuhani Mukubwa. Wakasimamisha Petro na Yoane mbele yao na kuwauliza: “Ni kwa uwezo gani au kwa jina la nani ninyi mumefanya jambo lile?” Halafu Petro akiwa amejazwa na Roho Mutakatifu, akawajibu: “Ninyi wasimamizi wa watu, nanyi wazee: Sisi tunasambishwa leo juu ya wema tuliomutendea mutu huyu aliyekuwa kiwete na juu ya namna alivyoponyeshwa. Kwa hiyo, ninyi wote pamoja na Waisraeli wote mujue vizuri kwamba mutu huyu anayesimama mbele yenu akiwa muzima kabisa, ni kwa uwezo wa jina la Yesu Kristo wa Nazareti, yule muliyemutundika juu ya musalaba, lakini Mungu amemufufua. Yeye ndiye Maandiko Matakatifu yanayosema hivi juu yake: ‘Jiwe lililokataliwa na ninyi wajengaji, limekuwa sasa jiwe kubwa la musingi.’ “Hivi hakuna anayeweza kuokolewa kwa njia ya mutu mwingine yeyote, kwa maana katika dunia nzima hakuna jina lingine lolote watu walilopewa lenye uwezo wa kuwaokoa.” Wajumbe wa Baraza Kubwa walishangaa sana kuona namna Petro na Yoane walivyosema bila woga na kujua kwamba walikuwa watu wasiojulikana na wasiokuwa na elimu. Wakatambua kwamba walikuwa pamoja na Yesu. Lakini kufuatana na vile walivyomwona mutu yule aliyeponyeshwa akisimama pale pamoja nao, wakakosewa na la kusema. Basi wakawaamuru watoke katika Baraza Kubwa na kwenda inje, nao wakaulizana shauri wao kwa wao, wakisema: “Tutafanya nini na watu hawa? Wakaaji wote wa Yerusalema wanajua kwamba wameonyesha vitambulisho, nasi hatuwezi kukana jambo lile. Lakini kwa kuzuiza habari za jambo lililotokea zisisambae zaidi kati ya watu, tuwakataze kwa ukali wasiendelee tena kusema na mutu yeyote wakitaja jina la Yesu.” Kisha wakawaita tena na kuwakataza kabisa kusema na kufundisha kwa jina la Yesu. Lakini Petro na Yoane wakawajibu: “Muamue ninyi wenyewe, ni haki mbele ya Mungu kuwatii ninyi kuliko kumutii Mungu? Kwa maana sisi hatuwezi kuacha kusema juu ya mambo tuliyoyaona na kuyasikia.” Kisha wale wakubwa wa baraza wakawakataza tena kwa ukali na kuwaachilia kwenda. Hawakupata njia ya kuwaazibu kwa maana watu wote walikuwa wakimusifu Mungu kwa ajili ya jambo lile lililotendeka. Naye yule mutu aliyeponyeshwa kwa njia ya kitambulisho hiki, alikuwa na umri wa miaka zaidi ya makumi ine. Petro na Yoane walipofunguliwa wakarudi kwa wenzao na kuwaelezea maneno yote wakubwa wa makuhani na wasimamizi wa watu waliyowaambia. Nao waliposikia habari hii, wote wakamwomba Mungu kwa nia moja, wakisema: “Ee Bwana, ni wewe uliyeumba mbingu, dunia na bahari na vitu vyote vinavyokuwa ndani yao. Ni wewe uliyesema maneno haya kwa njia ya Roho Mutakatifu kwa kinywa cha mutumishi wako babu yetu mukubwa Daudi: ‘Kwa nini mataifa wanafanya fujo, na kwa nini watu wanafanya mipango ya ovyo? Wafalme wanajikusanya, wakubwa wanafanya shauri wapate kumwasi Bwana, naye Kristo aliyemuchagua.’ “Ndiyo, ni kweli mufalme Herode, naye mutawala Pontio Pilato walikusanyika katika muji huu pamoja na Waisraeli na watu wa mataifa mengine kwa kufanya shauri baya juu ya mutumishi wako mutakatifu Yesu, uliyemuchagua kuwa Kristo. Hivi walitimiza mambo uliyokuwa umekusudia tangu zamani kwa uwezo wako na kwa mapenzi yako. Na sasa Ee Bwana, angalia vitisho vyao. Basi utuwezeshe sisi watumishi wako tupate kutangaza neno lako kwa uhodari kabisa. Utumie nguvu zako kwa kuponyesha watu, kwa kufanya maajabu na vitambulisho kwa uwezo wa jina la mutumishi wako mutakatifu Yesu.” Walipokwisha kuomba, nafasi ile walipokuwa wakikusanyika ikatikisika. Nao wote wakajazwa na Roho Mutakatifu na kuanza kutangaza Neno la Mungu kwa uhodari. Kundi lote la waamini walikuwa na roho moja na nia moja. Hakuna hata mumoja wao aliyehesabia mali yake kuwa yake mwenyewe, lakini walishirikiana katika vitu vyote. Nao mitume walishuhudia ufufuko wa Bwana Yesu kwa uwezo mukubwa, na Mungu akawabariki wote sana. Hakuna hata mutu mumoja kati ya wanafunzi aliyekuwa mukosefu. Kwa maana wale waliokuwa na mashamba au nyumba waliziuzisha na kuleta feza waliyopata kwa mikono ya mitume. Nao walizigawanya kwa watu wote kufuatana na mahitaji ya kila mumoja. Na kulikuwa Mulawi mumoja muzaliwa wa kisanga cha Kipuro, jina lake Yosefu. Mitume walimwita kwa jina lingine la Barnaba, maana yake “Mwenye kutia moyo.” Mutu huyu aliuzisha shamba alilokuwa nalo, na kuleta feza alizopata kwa mikono ya mitume. Vilevile kulikuwa mutu mwingine mumoja aliyeitwa Anania. Yeye alipokwisha kupatana na muke wake Safira, akauzisha shamba lake. Lakini akaficha sehemu ya feza alizopata na kuleta sehemu iliyobaki kwa mikono ya mitume. Muke wake alijua maneno hayo yote. Basi Petro akamwuliza: “Anania, namna gani Shetani amekuingia hata akakusemesha uongo mbele ya Roho Mutakatifu na kuficha sehemu ya feza ulizopata ulipouzisha lile shamba? Mbele haujauzisha lile shamba, si lilikuwa mali yako? Na nyuma ya kuliuzisha, feza ulizopata haungezitumia sawa unavyotaka? Basi namna gani ulikusudia kufanya jambo kama hili? Haukusema uongo mbele ya watu, lakini mbele ya Mungu!” Anania aliposikia maneno hayo, mara moja akaanguka chini na kufa. Na wote waliosikia habari ile wakashikwa sana na woga. Kisha vijana wakakuja, wakafunika maiti yake wakamubeba mbali na muji na kumuzika. Kulipopita karibu saa tatu, muke wake akafika pasipo kujua mambo yaliyotokea. Petro akamwuliza: “Uniambie, hii ndiyo jumla ya feza mulizopata mulipouzisha shamba lenu?” Akamujibu: “Ndiyo, ni hii.” Halafu Petro akamwambia: “Namna gani mulipatana kwa kumupima Roho wa Bwana? Sikiliza! Wale wanaotoka kumuzika mume wako wamefika hapa kwenye mulango, nao watakupeleka vilevile.” Mara moja Safira akaanguka chini mbele ya Petro na kufa. Halafu wale vijana wakaingia ndani, wakamukuta amekwisha kufa. Basi wakamubeba mbali na muji na kumuzika kule karibu na mume wake. Halafu, kanisa lote na wote waliosikia habari ile wakashikwa sana na woga. Mitume walifanya maajabu na vitambulisho vingi katikati ya watu. Waamini wote walizoea kukusanyika katika Baraza wanaloliita La Solomono. Na hapakukuwa hata mutu mumoja asiyekuwa mwamini aliyesubutu kujiunga nao, lakini hata hivi wanafunzi walisifiwa sana na watu. Hesabu ya watu waliomwamini Bwana, wanaume na wanawake, ilizidi kuongezeka sana. Na kufuatana na mambo yote yaliyotokea, watu waliwapeleka wagonjwa katika barabara, wakiwalalisha juu ya mikeka na vipoyi kusudi Petro atakapopita, kivuli chake kipate tu kufika kwenye wamoja wao. Watu wengi vilevile kutoka miji inayokuwa pembeni ya Yerusalema walikusanyika, wakiwaleta wagonjwa na watu wanaoteswa na pepo, na wote wakaponyeshwa. Halafu Kuhani Mukubwa na washiriki wake wote, ndio watu wa chama cha Wasadukayo, wakawaonea mitume wivu. Basi wakafunga mitume na kuwapeleka ndani ya nyumba kubwa ya kifungo. Lakini usiku malaika wa Bwana akafungua milango ya kifungo, akawaondosha mitume mule na kuwaambia: “Mwende ndani ya hekalu na mutangaze kwa watu maneno yote yanayoelekea uzima mupya.” Na sawa vile walivyoambiwa, asubui mapema wakaingia ndani ya hekalu, na kuanza kuwafundisha watu. Kuhani Mukubwa na wale washiriki walipofika, wakawakusanya wasimamizi wote wa Waisraeli kwa kufanya mukutano wa Baraza Kubwa. Nao wakawatuma watu kwenye kifungo kwa kuwaleta mitume. Lakini wale walinzi waliotumwa walipofika, hawakuwakuta mitume ndani ya kifungo. Basi wakarudi na kutoa habari hii: “Tulikuta kifungo kimefungwa vizuri na waaskari walinzi wakichunga milango. Lakini wakati tulipofungua milango hatukuona mutu ndani.” Mukubwa wa walinzi wa hekalu na wakubwa wa makuhani waliposikia habari hii, wakakuwa na wasiwasi sana, wakijiuliza ni nini itakayotokea. Halafu mutu mumoja akakuja, na kuwaambia: “Wale watu muliowatia ndani ya kifungo wako katika hekalu wakiwafundisha watu.” Basi mukubwa wa walinzi wa hekalu akaenda pamoja na watumishi wake, akawaleta mitume. Lakini hawakuwakamata kwa kinguvu kwa sababu waliogopa watu wasiwatupie mawe. Walipokwisha kuwaleta, wakawasimamisha mbele ya Baraza Kubwa. Naye Kuhani Mukubwa akaanza kuwasambisha, akiwaambia: “Tuliwakataza kwa nguvu musifundishe tena kwa jina la mutu huyu. Na sasa mumeeneza mafundisho yenu katika Yerusalema yote, nanyi munataka kutubebesha lazima ya kifo chake.” Petro na mitume wengine wakajibu: “Inatupasa sisi kumutii Mungu kuliko watu! Mungu wa babu zetu alimufufua Yesu, yule ninyi muliyemwua kwa kumutundika juu ya musalaba. Mungu alimupa utukufu na kumwikalisha na mamlaka karibu naye na kumuweka kuwa Mutawala na Mwokozi. Na hivi Waisraeli wataweza kugeuka toka zambi zao na Mungu atawasamehe. Na sisi ni washuhuda wa mambo hayo, naye Roho Mutakatifu ambaye Mungu aliwapa wale wanaomutii, anayashuhudia vilevile.” Wajumbe wa lile Baraza Kubwa waliposikia maneno hayo, wakakasirika sana na kutaka kuwaua mitume. Lakini Mufarisayo mumoja, jina lake Gamalieli, aliyekuwa mwalimu wa Sheria na aliyeheshimiwa sana na watu wote, akasimama katika baraza na kuamuru mitume wapelekwe inje kwa muda. Kisha akawaambia watu wa baraza: “Ninyi wanainchi wenzangu Waisraeli, muangalie vizuri jambo hili munalotaka kuwatendea watu hawa. Haijapita siku nyingi kulitokea mutu mumoja aliyeitwa Teuda. Akajidai kuwa mutu mukubwa, na karibu watu mia ine walijiunga naye. Lakini akauawa na wanafunzi wake wote wakasambazwa na kutosemekana tena. Nyuma yake, katika siku zile walipofanya hesabu ya watu, kulitokea Yuda wa jimbo la Galilaya. Huyo naye aliwavuta watu wengine kwa kumufuata. Lakini yeye vilevile aliuawa na wanafunzi wake wote wakasambazwa. Na sasa mimi ninawashauria ninyi, musiwafuatilie watu hawa, muwaache wajiendee. Kwa maana ikiwa mupango huu na hii kazi yao vimeanzishwa na mwanadamu, sherti vitaharibika. Lakini ikiwa vimeanzishwa na Mungu, hamutaweza kuwazuiza. Basi mujiangalie vizuri musikuje kuonekana kuwa munapigana na Mungu!” Wajumbe wa baraza wakakubali shauri la Gamalieli. Halafu wakawaita mitume, wakawapiga fimbo na kuamuru wasifundishe tena kwa jina la Yesu. Kisha wakawaacha kwenda. Basi mitume wakatoka katika baraza, wakifurahi sana kwa sababu walistahili kuzarauliwa kwa kuteswa kwa ajili ya Yesu. Na kila siku, katika hekalu na katika nyumba mbalimbali, hawakuacha kufundisha na kuhubiri Habari Njema kwamba Yesu ni Kristo. Katika siku zile, kufuatana na jinsi hesabu ya wanafunzi wa Yesu ilivyokuwa ikizidi kuongezeka, kulitokea manunguniko kati ya Wayuda waliosema Kigriki na Wayuda waliosema Kiebrania. Wale waliosema Kigriki walinungunika kwa sababu wajane wao walisahauliwa wakati wa kugawanya vifaa vya kila siku. Kwa hiyo wale mitume kumi na wawili wakafanya mukutano wa kundi lote la wanafunzi, na kuwaambia: “Haifai sisi tuache kuhubiri Neno la Mungu kwa ajili ya kushugulika na kazi ya kugawanya vyakula. Hivi wandugu, muwachague wanaume saba kati yenu wenye ushuhuda muzuri, wenye kujazwa na Roho Mutakatifu na wenye hekima, kusudi tuwaweke kwa kazi hii. Na sisi kwa ngambo yetu tutajitolea kwa kuomba Mungu na kuhubiri neno lake.” Kundi lote likapendezwa na shauri hilo. Nao wakawachagua watu hawa: Stefano, mutu mwenye imani sana na aliyejazwa na Roho Mutakatifu, Filipo, Porokoro, Nikanora, Timoni, Permena na Nikolao, mutu wa Antiokia aliyekuwa amegeuka zamani kufuata dini ya Kiyuda. Kisha wakawaweka mbele ya mitume, nao wakaomba na kuweka mikono juu yao. Basi Neno la Mungu likazidi kuenea katika Yerusalema na hesabu ya wanafunzi ikaongezeka sana kule na makuhani wengi wakaamini. Stefano alijaliwa sana na neema ya Mungu na alikuwa na uwezo mwingi, naye alifanya maajabu na vitambulisho vikubwa katikati ya watu. Lakini kukatokea watu wamoja waliopingana na Stefano. Watu hawa walikuwa wa nyumba ya kuabudia iliyojulikana kwa jina la “Wenye Uhuru.” Nao walitoka katika inchi ya Kurene na ya Alesanduria, na kutoka jimbo la Kilikia na la Azia. Watu hawa wakaanza kubishana na Stefano lakini hawakuweza kumushinda kwa sababu ya hekima yake na kwa sababu ya Roho Mutakatifu aliyemwongoza kusema. Halafu wakawashawishi watu wamoja kusudi waseme kwamba wamemusikia Stefano akisema maneno ya kumutukana Musa na Mungu. Basi wakawachochea watu, wazee, na walimu wa Sheria. Nao wakamufikia Stefano, wakamukamata na kumupeleka mbele ya Baraza Kubwa. Kisha wakaleta washuhuda wa uongo waliosema: “Mutu huyu hachoki na kusema maneno ya kutukana hili hekalu letu takatifu pamoja na Sheria ya Musa! Kwa maana tumemusikia akisema kwamba huyu Yesu wa Nazareti ataharibu hekalu hili na kugeuza desturi tulizopokea toka kwa Musa.” Na wote waliohuzuria katika lile Baraza wakamukazia Stefano macho, wakaona uso wake unafanana sawa na uso wa malaika. Halafu Kuhani Mukubwa akamwuliza Stefano: “Maneno haya wanayokushitakia ni ya kweli?” Stefano akamujibu: “Wandugu zangu na wababa zangu, munisikilize! Mungu mwenye utukufu alimutokea babu yetu mukubwa Abrahamu wakati alipokuwa angali katika inchi ya Mesopotamia, mbele hajahamia katika muji Harani. Mungu alimwambia: ‘Toka katika inchi yako na uache wandugu zako, uende katika inchi nitakayokuonyesha.’ Basi Abrahamu akatoka katika inchi ya Wababeli akaenda kukaa Harani. Kisha kufa kwa baba yake, Mungu akamuhamisha tena, akakuja kukaa katika inchi hii munayoishi ndani yake sasa. Kule Mungu hakumupa Abrahamu hata sehemu ndogo ya shamba inayokuwa kama kikanyagio cha muguu kuwa urizi wake, lakini alimwahidi kwamba atamupa inchi hii kuwa urizi wake na wa wazao wake watakaoishi nyuma yake. Wakati ule, alikuwa hana mutoto. Mungu alimwambia: ‘Wazao wako wataishi katika inchi ya kigeni, na kule watafanywa kuwa watumwa, nao watateswa kwa muda wa miaka mia ine. Lakini mimi nitaazibu taifa lile litakalowafanya kuwa watumwa. Kisha nitawaondoa katika inchi ile, nao wataniabudu kwenye nafasi hii.’ Halafu Mungu akafanya agano na Abrahamu, na kitambulisho cha kuhakikisha kwamba limeshikwa kilikuwa kutahiriwa. Kwa hiyo Abrahamu akamutahiri mwana wake Isaka alipotimiza siku nane za kuzaliwa. Naye Isaka akamutahiri mwana wake Yakobo, na Yakobo akawatahiri wana wake kumi na wawili waliokuwa babu zetu wakubwa. “Wale babu wakamwonea Yosefu wivu hata wakamwuzisha kuwa mutumwa katika inchi ya Misri. Lakini Mungu akamulinda, akamwokoa toka katika taabu yote aliyopata. Mungu akamujalia neema, apate kupendwa na Mufalme wa Misri na kuonekana kuwa mwenye hekima mbele yake. Mufalme yule akamuweka kuwa musimamizi wa inchi yake na wa nyumba yake yote. Halafu kukatokea njaa kubwa na mateso mengi katika inchi yote ya Misri na ya Kanana, nao babu zetu wakakuwa katika ukosefu wa chakula. Yakobo alipopata habari kwamba kuna ngano katika Misri, akawatuma babu zetu kule mara ya kwanza. Kwa safari ya pili, Yosefu akajitambulisha kwa wandugu zake, naye Mufalme wa Misri akapata kujua jamaa ya Yosefu. Kisha Yosefu akatuma wajumbe kwenda kumwita baba yake Yakobo pamoja na jamaa yake yote wafike Misri. Nao wote kwa jumla walikuwa makumi saba na tano. Halafu Yakobo akashuka kwenda Misri, naye akakaa kule pamoja na babu zetu. Maiti zao zikapelekwa katika jimbo la Sekemu na kuzikwa katika kaburi lile Abrahamu alilonunua kwa feza kutoka kwa wazao wa Hemora. “Siku za kutimiza ahadi Mungu aliyotoa kwa Abrahamu zilipokaribia, hesabu ya watu wa taifa letu kule Misri ikaongezeka hata ikazidika sana. Halafu kukakuwa mufalme mwingine wa inchi ya Misri, asiyemujua Yosefu. Mufalme huyo akatendea taifa letu kwa udanganyifu, akawatesa babu zetu hata akawalazimisha kuwatupilia watoto wao wachanga kusudi wakufe. Na katika siku zile Musa akazaliwa, naye alikuwa mutoto muzuri sana. Alilelewa muda wa miezi mitatu katika nyumba ya baba yake. Alipowekwa inje, binti ya Mufalme wa Misri akamutwaa na kumulea kama mutoto wake mwenyewe. Musa akafundishwa mambo yote ya hekima ya Wamisri, akakuwa mwenye uwezo sana katika masemi yake na matendo yake. “Wakati Musa alipokuwa na umri wa miaka makumi ine, akakusudia kwenda kuwatembelea wandugu zake Waisraeli. Kule akamwona Mumisri mumoja akimutendea mumoja wa wale wandugu zake vibaya. Basi akamusaidia yule aliyeonewa; akalipiza kisasi kwa kumwua yule Mumisri. Musa alizani kwamba wandugu zake wataelewa kwamba Mungu atawaokoa kwa njia yake, lakini hawakuelewa vile. Kesho yake akawakutana Waisraeli wawili wakipigana, naye akajaribu kuwaamua, akiwaambia: ‘Warafiki, ninyi ni wandugu; kwa sababu gani munatendeana vibaya?’ Lakini yule aliyekuwa akimutendea mwenzake vibaya akamusukuma Musa pembeni akisema: ‘Nani aliyekuweka wewe kuwa mukubwa na mwamuzi wetu? Unataka kuniua sawa vile ulivyomwua yule Mumisri jana?’ Kwa ajili ya maneno hayo akakimbia na kwenda kukaa katika inchi ya Midiani. Na kule akazaa wana wawili. “Kulipopita miaka makumi ine, malaika wa Bwana akamutokea Musa katikati ya kichaka kilichokuwa kikiwaka moto katika jangwa karibu na mulima Sinai. Musa alipoona jambo hilo akashangaa sana, naye aliposogea karibu kusudi aangalie, akasikia sauti ya Bwana ikisema: ‘Mimi ni Mungu wa babu zako, Mungu wa Abrahamu, Isaka na Yakobo.’ Musa akatetemeka kwa woga wala hakusubutu kuendelea kuangalia. Halafu Bwana akamwambia: ‘Vua viatu vyako, kwa sababu hapa unaposimama ni pahali patakatifu. Hakika nimeona namna watu wangu Waisraeli wanavyoteswa katika inchi ya Misri. Nimesikia kilio chao nami nimeshuka kwa kuwaokoa. Sasa kuja, nitakutuma kule Misri.’ “Huyu Musa ndiye yule Waisraeli waliyemukataa, wakisema: ‘Nani aliyekuweka wewe kuwa mukubwa na mwamuzi?’ Mungu alimutuma kuwa mukubwa na mukombozi wao, akisaidiwa na yule malaika aliyemutokea katikati ya kichaka kinachowaka moto. Yeye ndiye aliyewaongoza Waisraeli toka Misri akifanya maajabu na vitambulisho katika inchi ile, na kwenye bahari Nyekundu na katika jangwa kwa muda wa miaka makumi ine. Ni yule yule Musa ndiye aliyewaambia watu wa Israeli: ‘Mungu atawatumia ninyi nabii anayekuwa sawa mimi, toka katika taifa lenu.’ Na wakati ule kulipokuwa mukutano wa Waisraeli katika jangwa, yeye alikuwa pale pamoja na babu zetu na yule malaika aliyesema naye kwenye mulima Sinai. Na ni yeye aliyefunuliwa ujumbe wa Mungu unaoleta uzima na kuutangaza kwetu. “Babu zetu hawakutaka kumusikiliza Musa, wakamukataa na kutamani kurudi Misri. Wakamwambia Haruni: ‘Ututengenezee sanamu itakayotuongoza, kwa maana hatujui jambo gani lililomupata yule Musa aliyetuondoa Misri.’ Katika siku zile wakajitengenezea sanamu ya mwana-ngombe, wakaitambikia na kufurahia kitu hicho walichojifanyia wao wenyewe. Basi Mungu akajitenga mbali nao, akawaacha waabudu nyota, jua na mwezi kufuatana na maneno haya yaliyoandikwa katika kitabu cha manabii: ‘Ninyi watu wa Israeli, si mimi muliyemuchinjia nyama na kumutolea sadaka zingine kwa muda wa ile miaka makumi ine katika jangwa. Mulitembea mukibeba hema ya mungu wenu Moleki nayo sanamu ya nyota ya mungu wenu Refani. Mulijitengenezea sanamu hizo kusudi muziabudu. Kwa hiyo nitawahamisha mbali kupita muji Babeli.’ “Kule katika jangwa babu zetu walikuwa na ile hema inayokuwa na vibao vya agano ndani yake. Hema ile ilikuwa imetengenezwa kama vile Mungu alivyomwagiza Musa, na mufano ule alioonyeshwa. Kisha ile hema ikaachwa kwa kizazi cha babu zetu kilichofuata. Nao wakaibeba chini ya uongozi wa Yoshua mpaka waliponyanganya inchi ya mataifa yale Mungu aliyofukuza mbele ya kufika kwao. Nayo ikabaki katika inchi mpaka katika siku za Daudi. Mungu akamujalia Daudi neema hata akamwomba yeye Mungu wa Yakobo ruhusa ya kumujengea nyumba. Ingawa vile mwana wake Solomono ndiye aliyemujengea nyumba. “Lakini Mungu Mukubwa hakai ndani ya nyumba zilizojengwa na watu kama vile inavyosemwa katika maandiko haya ya manabii: ‘Mbingu ni kiti changu cha kifalme, nayo dunia ni kiti changu cha kupumzishia miguu. Basi ni nyumba gani munayoweza kunijengea? Au ni nafasi gani munaweza kuniwekea makao? Ni mimi peke yangu niliyeumba vitu hivi vyote!’ “Ninyi watu wagumu! Ninyi wenye roho ya kipagani na masikio yanayofungana! Siku zote munapingana na Roho Mutakatifu sawa vile babu zenu walivyofanya! Ni nani kati ya manabii ambaye babu zenu walikosa kumutesa? Waliwaua wale waliotabiri zamani habari za kuja kwa Mwenye Haki. Na sasa mumemutoa na kumwua. Mungu aliwatolea ninyi Sheria yake kwa njia ya wamalaika, lakini hamukuitii.” Wajumbe wa Baraza Kubwa waliposikia maneno hayo, wakakasirika sana na kumusagia Stefano meno. Lakini Stefano akijazwa na Roho Mutakatifu, akakaza macho kuelekea mbingu akaona mwangaza wa utukufu wa Mungu naye Yesu akisimama na mamlaka karibu na Mungu. Naye Stefano akasema: “Ninaona mbingu zimefunguliwa wazi, naye Mwana wa Mutu akisimama na mamlaka karibu na Mungu.” Basi wale wajumbe wakafunga masikio yao, wakapiga kelele kwa nguvu na kumurukia wote pamoja. Wakamukokota na kumupeleka mbali na muji na kuanza kumutupia mawe kusudi wamwue. Wale washuhuda wakavua nguo zao na kuziwekesha kijana mumoja Saulo. Walipokuwa wakimutupia mawe, Stefano akaomba akisema: “Ee Bwana Yesu, pokea roho yangu.” Kisha akapiga magoti, akalalamika, akisema: “Bwana, usiwahesabie zambi hii.” Na nyuma ya kusema maneno haya, akakufa. Naye Saulo alikuwa amekubali kwamba Stefano anastahili kuuawa. Siku ile ile kanisa lililokuwa katika Yerusalema lilianza kupata mateso makubwa. Waamini wote walisambaa katika Yudea na Samaria, isipokuwa mitume tu. Watu wenye kuogopa Mungu wakamuzika Stefano na kumufanyia kilio kikubwa. Lakini Saulo aliendelea kuteketeza kanisa, akiingia nyumba kwa nyumba, na kuwakamata waamini, wanaume na wanawake, na kwenda kuwatupa katika kifungo. Wale waamini waliosambaa walikwenda popote wakitangaza Habari Njema. Naye Filipo akaenda katika muji mukubwa wa Samaria na kuwahubiri wakaaji wake juu ya Kristo. Makundi ya watu waliposikia maneno yale Filipo aliyosema na kuona vitambulisho alivyoonyesha, wote walimusikiliza kwa nia moja na kwa uangalifu. Maana pepo walitoka ndani ya watu wengi wakilalamika kwa sauti kubwa, na watu wengi wenye kupooza pamoja na viwete waliponyeshwa vilevile. Hivi kukakuwa furaha kubwa katika muji ule. Na kulikuwa mutu mumoja aliyeitwa Simoni aliyekuwa akikaa katika muji ule ule tangu mbele. Yeye alikuwa akifanya mambo ya uchawi na kuwashangaza watu wa Samaria. Alijidai kuwa yeye ni mutu mukubwa. Watu wote, tangia wadogo mpaka wakubwa walimusikiliza kwa uangalifu, wakisema: “Mutu huyu ndiye ule uwezo wa Mungu unaoitwa ‘Uwezo Mukubwa.’ ” Hakika walimusikiliza vizuri kwa sababu aliwashangaza kwa muda wa siku nyingi kwa njia ya uchawi wake. Lakini walipoamini Habari Njema ambayo Filipo alihubiri juu ya Ufalme wa Mungu na juu ya Yesu Kristo, wanaume na wanawake wakabatizwa. Hata Simoni vilevile akaamini na kubatizwa. Na nyuma ya pale alishikamana na Filipo, naye alishangaa sana alipoona kitambulisho kikubwa na miujiza iliyokuwa ikifanyika. Mitume waliokuwa Yerusalema waliposikia kwamba wakaaji wa Samaria wamekubali Neno la Mungu, wakawatumia Petro na Yoane. Walipofika Samaria, wakawaombea waamini wapate kupokea Roho Mutakatifu. Kwa maana Roho Mutakatifu alikuwa bado hajashuka hata juu ya mumoja wao; walikuwa tu wamebatizwa kwa jina la Bwana Yesu. Halafu Petro na Yoane wakaweka mikono juu yao, nao wakapokea Roho Mutakatifu. Simoni alipoona kwamba wanafunzi wamepokea Roho Mutakatifu kwa njia ya kuwekewa mikono ya mitume, akaletea Petro na Yoane feza na kuwaambia: “Munipe nami vilevile uwezo huu; kusudi yeyote nitakayeweka mikono juu yake, apate kupokea Roho Mutakatifu.” Lakini Petro akamujibu: “Feza yako ipotelee mbali pamoja nawe, kwa sababu umezani kwamba unaweza kununua ile zawadi ya Mungu kwa njia ya feza! Wewe hauna sehemu wala haki yoyote katika jambo hili, kwa sababu moyo wako si mukamilifu mbele ya Mungu. Basi ugeuke toka katika zambi zako na umwombe Bwana, labda atakusamehe kwa ajili ya mawazo ya namna hii. Kwa maana ninaona kwamba umejaa uchungu sana nawe umefungwa na zambi.” Halafu Simoni akawaambia Petro na Yoane: “Muniombee ninyi wenyewe kwa Bwana, kusudi lisinipate hata neno moja kati ya maneno haya muliyosema.” Kisha kushuhudia na kuhubiri neno la Bwana, Petro na Yoane wakarudi Yerusalema wakitangaza Habari Njema katika vijiji vingi vya Samaria. Malaika wa Bwana akamwambia Filipo: “Ujitayarishe na uende upande wa kusini kupitia njia inayotelemuka toka Yerusalema kwenda katika muji Gaza, nayo ni njia watu wasiyozoea kupitia.” Basi Filipo akajitayarisha na kwenda. Alipokuwa katika njia, mara moja akakutana na towashi mumoja Mwetiopia. Mutu huyu alikuwa mukubwa, alishugulika na kazi ya usimamizi wa mali zote za malkia Kandake wa Etiopia. Yeye alikuwa amekwenda Yerusalema kwa kumwabudu Mungu, na sasa alikuwa katika safari ya kurudi kwake. Alikuwa akiikaa ndani ya gari lake akisoma katika kitabu cha nabii Isaya. Roho Mutakatifu akamwambia Filipo: “Endelea, usogee karibu na lile gari.” Filipo akaenda mbio karibu na gari, naye akamusikia yule mukubwa akisoma katika kitabu cha nabii Isaya. Filipo akamwuliza: “Unaelewa maneno unayoyasoma?” Naye akamujibu: “Nitayaelewa namna gani pasipo mutu wa kunielezea?” Halafu akamwomba Filipo apande na kuikaa karibu naye ndani ya gari. Na sehemu ya Maandiko aliyokuwa akisoma ni hii: “Alipelekwa kama kondoo kwenda kuchinjwa, kama mwana-kondoo anayenyamaza mbele ya mwenye kumukata manyoya. Yeye hakufungua kinywa chake. Alinyenyekezwa na kuhukumiwa bila haki. Hakuna mutu atakayeweza kueleza habari za kizazi chake, maana maisha yake yameondolewa katika dunia.” Yule mukubwa akamwuliza Filipo: “Ninakusihi uniambie, nabii huyu anasema juu ya nani? Ni juu yake mwenyewe au juu ya mutu mwingine?” Basi Filipo akaanza na sehemu ile ile ya maandiko, akamwelezea Habari Njema juu ya Yesu. Walipokuwa wakiendelea na safari, wakafika kwenye nafasi moja kwenye maji, yule mukubwa akasema: “Hapa kuna maji. Ni kitu gani kinachonizuiza nisibatizwe?” [ Filipo akamwambia: “Kama unaamini kwa moyo wako wote, unaweza kubatizwa.” Yule mukubwa akamujibu: “Ninaamini kwamba Yesu Kristo ni Mwana wa Mungu.”] Kisha akasimamisha gari. Filipo na yule mukubwa wakashuka wote wawili ndani ya maji na Filipo akamubatiza. Walipotoka ndani ya maji, kwa rafla Roho wa Bwana akamutowesha Filipo, na yule mukubwa hakumwona tena, lakini akaongeza safari yake katika furaha. Filipo akajikuta amekwisha kuwa katika muji Azoto. Kisha akapita katika miji yote akihubiri Habari Njema, mpaka alipofika katika muji Kaisaria. Katika siku zile zile, Saulo aliendelea na vitisho vikali vya kuwaua wanafunzi wa Bwana. Siku moja akamwendea Kuhani Mukubwa na kumwomba amwandikie barua za kumutambulisha katika nyumba za kuabudia za muji Damasiki. Katika barua hizo, Saulo alipewa ruhusa kwamba akiona watu wanaofuata Njia ya Bwana, ikiwa wanaume au wanawake, awafunge na kuwapeleka Yerusalema. Alipokuwa katika safari karibu kufika Damasiki, kwa rafla mwangaza toka mbinguni ukamuzunguka. Akaanguka chini, akasikia sauti ikimwambia: “Saulo, Saulo, sababu gani unanitesa?” Naye akauliza: “Wewe ni nani, Bwana?” Na Bwana akajibu: “Mimi ni Yesu unayemutesa. Lakini simama, uingie katika muji, na mule watakuambia jambo unalopaswa kufanya.” Nao watu waliosafiri pamoja na Saulo wakasimama na kubaki kimya kwa ajili ya mushangao, kwa maana walisikia sauti lakini hawakuona mutu. Saulo akasimama wima, na ingawa macho yake yalikuwa wazi hakuweza kuona kitu. Halafu wakamushika mukono na kumwongoza mpaka ndani ya muji Damasiki. Akabaki muda wa siku tatu pasipo kuona, naye hakukula wala kunywa kitu. Na kule Damasiki kulikuwa mwanafunzi mumoja wa Yesu jina lake Anania. Bwana akamutokea katika maono, akamwita akisema: “Anania!” Naye akamwitikia, akisema: “Bwana, mimi niko hapa.” Bwana akamwambia: “Kwenda katika barabara wanayoita ‘Yenye Kunyooka,’ uingie ndani ya nyumba ya Yuda, na mule umutafute mutu wa muji wa Tarso anayeitwa Saulo, utamukuta akiomba. Yeye ameona katika maono mutu mumoja anayeitwa Anania, akiingia ndani ya nyumba na kuweka mikono juu yake kusudi apate kuona tena.” Anania akajibu: “Bwana, nimekwisha kusikia watu wengi wakisema habari za mutu huyo, wakieleza mabaya aliyowatendea watu wako watakatifu wanaokuwa Yerusalema. Na hata huku yuko na mamlaka aliyopewa na wakubwa wa makuhani kusudi afunge wote wanaoomba kwa jina lako.” Lakini Bwana akamwambia: “Kwenda tu, kwa maana nimemuchagua mutu huyu kwa kunitumikia, kusudi atangaze jina langu kwa mataifa, kwa wafalme na kwa Waisraeli. Nami nitamwonyesha mateso ya namna gani atakayopaswa kupata kwa ajili yangu.” Basi Anania akaenda. Alipofika ndani ya nyumba ambamo Saulo alikuwa, akaweka mikono juu yake na kumwambia: “Ndugu Saulo, Bwana Yesu aliyekutokea katika njia ulipokuwa ukikuja huku, amenituma kusudi upate kuona tena na kujazwa na Roho Mutakatifu.” Na pale pale vitu vilivyokuwa kama magamba vikaanguka toka ndani ya macho ya Saulo, naye akapata tena kuona. Halafu akasimama na kubatizwa. Kisha akakula chakula, na kupata nguvu tena. Saulo alikaa siku chache pamoja na wanafunzi waliokuwa Damasiki. Na bila kukawia akaanza kuhubiri katika nyumba za kuabudia, akitangaza kwamba Yesu ni Mwana wa Mungu. Wote waliomusikia walishangaa, wakisema: “Si mutu huyu ndiye aliyewatesa vikali kule Yerusalema watu wanaoomba kwa jina la Yesu? Hakika amefika huku nako kusudi awafunge watu kama hao na kuwapeleka kwa wakubwa wa makuhani.” Lakini Saulo akazidi kuhubiri na uwezo, akawashinda Wayuda waliokaa Damasiki akihakikisha wazi kwao kwamba Yesu ndiye Kristo. Na kulipokwisha kupita siku nyingi, Wayuda wakafanya shauri la kumwua Saulo, lakini Saulo akavumbua shauri lile. Nao walichunga milango ya kuingilia ndani ya muji ule muchana na usiku kusudi wamwue, lakini siku moja usiku wanafunzi wa Saulo wakamutwaa, wakamuweka ndani ya kitunga na kumutelemusha na kamba inje ya ukuta. Saulo alipofika Yerusalema, alijaribu kujiunga na wanafunzi wengine, lakini wote walimwogopa, kwa sababu hawakusadiki kwamba amekwisha kugeuka mwanafunzi. Basi Barnaba akamutwaa na kumupeleka kwa mitume. Akawaelezea namna Saulo alivyomwona Bwana katika njia na jinsi Bwana alivyosema naye. Akawaelezea vilevile namna Saulo alihubiri kwa jina la Yesu pasipo woga katika Damasiki. Saulo akakaa pamoja nao, akaenda huku na huko katika muji Yerusalema akihubiri kwa jina la Yesu pasipo woga. Vilevile alisemezana na kubishana na Wayuda waliosema kigriki, lakini wao walitafuta njia ya kumwua. Wandugu walipopata habari ile, wakamupeleka mbali katika muji Kaisaria, na kutoka kule wakamutuma aende katika muji Tarso. Wakati ule, kanisa lilikuwa na amani katika Yudea yote, Galilaya na Samaria. Vilevile lilizidi kupata nguvu na kuendelea kumwogopa Bwana, nalo liliongezeka kwa musaada wa Roho Mutakatifu. Petro alipokuwa akipita fasi zote katika majimbo yale, siku moja akawatembelea wanafunzi walioishi katika muji wa Luda. Kule akamwona mutu mumoja mwenye ugonjwa wa kupooza aliyeitwa Ainea aliyeshindwa kutoka ndani ya kitanda kwa muda wa miaka minane. Petro akamwambia: “Ainea, Yesu Kristo anakuponyesha. Simama, ujitandikie kitanda chako wewe mwenyewe.” Na mara moja Ainea akasimama. Nao wakaaji wote wa Luda na bonde la Saroni walipoona jambo hilo wakamugeukia Bwana. Katika muji wa Yopa kulikuwa mwanafunzi mumoja mwanamuke aliyeitwa Tabita. (Katika kigriki ni “Dorika,” maana yake “Pongo”.) Mwanamuke huyu alikuwa akifanya matendo mengi mema na kuwasaidia wamasikini. Katika siku zile akapata ugonjwa, naye akakufa. Walipokwisha kunawisha maiti yake, wakailalisha ndani ya chumba cha gorofi. Na kwa kuwa muji Luda ulikuwa karibu na muji Yopa, wanafunzi walikuwa wamesikia kwamba Petro yuko kule. Kwa hiyo wakatuma kwake wajumbe wawili kwa kumwambia: “Tunakusihi, ufike huku kwetu bila kukawia.” Mara moja Petro akaenda pamoja nao. Naye alipofika wakamupeleka ndani ya chumba cha gorofi. Wajane wote wakamuzunguka Petro, wakilia na kumwonyesha kanzu na nguo zote Dorika alizowashonea wakati alipokuwa angali muzima. Petro akawaamuru watu wote waende inje, akapiga magoti na kuomba. Kisha akaelekea ile maiti na kusema: “Tabita, simama!” Halafu Tabita akafungua macho, na wakati alipomwona Petro akaamuka na kuikaa. Petro akamushika mukono na kumusimamisha wima. Kisha akawaita wanafunzi na wajane, akamupeleka mbele yao akiwa muzima. Na habari hii ikaenea katika muji wote wa Yopa, kwa hiyo watu wengi wakamwamini Bwana. Petro akakaa siku nyingi huko Yopa kwa fundi mumoja wa kutengeneza vitu vya ngozi, aliyeitwa Simoni. Katika muji Kaisaria, kulikuwa mutu mumoja jina lake Kornelio. Yeye alikuwa mukubwa wa kundi la waaskari lililoitwa “Kundi la Italia.” Yeye alikuwa mwenye kuogopa Mungu, naye alimwabudu Mungu pamoja na watu wote waliokuwa kwake. Aliwasaidia wamasikini wengi, naye alikuwa akimwomba Mungu siku zote. Siku moja, ilipokuwa saa tisa ya muchana, akaona maono. Aliona waziwazi malaika wa Mungu akiingia kwake na kumwambia: “Kornelio!” Kornelio akamukazia macho akiwa ameshikwa na woga, akamwuliza: “Bwana, ni nini?” Malaika akamujibu: “Mungu amesikia maombi yako na kupendezwa na misaada unayotoa kwa wamasikini, na kwa hiyo anakukumbuka. Basi sasa; uwatume watu Yopa waende kumwita mutu mumoja jina lake Simoni anayeitwa vilevile Petro. Anapanga kwa fundi mumoja wa kutengeneza vitu vya ngozi, anayeitwa Simoni. Nyumba yake iko pembeni ya bahari.” Yule malaika aliyesema na Kornelio alipoondoka, akawaita watu wawili kati ya watumishi wake na askari mumoja mwenye kuogopa Mungu, aliyekuwa mumoja wa wasimamizi wake wa kipekee. Na kisha kuwaelezea mambo yote yaliyotokea, akawatuma Yopa. Kesho yake karibu na saa sita ya muchana, hao watu watatu wakafika karibu na Yopa, saa ile Petro akapanda juu ya paa kwa kuomba. Naye akasikia njaa, na kuhitaji chakula. Walipokuwa wakimutengenezea chakula, akakuwa sawa amezimia. Akaona katika maono mbingu imefunguliwa wazi, na kitu kimoja kinachokuwa kama nguo kubwa kikishuka, kikitelemushwa mpaka chini, kikishikwa kwenye pembe zake ine. Na ndani yake kulikuwa kila namna ya nyama wenye miguu mine na wenye kutambaa pamoja na ndege. Kisha akasikia sauti ikimwambia: “Petro, simama. Chinja na ukule!” Lakini Petro akajibu: “Hapana, hata kidogo Ee Bwana! Mimi sijakula bado kitu chochote kisichoruhusiwa kukuliwa, wala chochote kinachohesabiwa kuwa kichafu.” Lakini ile sauti ikamurudilia, ikisema: “Vitu vilivyotakaswa na Mungu, usivihesabu kuwa vichafu.” Nayo maneno haya yakasikilika tena mara tatu, kisha chombo kile kikanyanyuliwa mbinguni. Petro alipokuwa angali na wasiwasi, naye akijiuliza juu ya maana ya maono yale, wale watu waliotumwa na Kornelio wakafika mbele ya mulango kwa maana walikuwa wamekwisha kujulishwa nafasi gani kunapokuwa nyumba ya Simoni. Wakapiga hodi wakiuliza kama Simoni anayeitwa vilevile Petro anapanga pale. Petro akiwa akifikiri juu ya maana ya yale maono, Roho Mutakatifu akamwambia: “Kuna watu watatu hapa wanaokutafuta. Basi, simama ushuke na kwenda pamoja nao pasipo kusita, kwa maana ni mimi niliyewatuma.” Halafu Petro akashuka na kuwaambia wale watu: “Ni mimi munayemutafuta. Mumekuja hapa kwa sababu gani?” Nao wakamujibu: “Tumetumwa hapa na Kornelio, mukubwa wa waaskari. Yeye ni mutu wa haki na mwenye kumutii Mungu, naye anasifiwa na Wayuda wote. Malaika mutakatifu amemutokea na kumwagiza akuite ufike kwake kusudi asikie maneno utakayomwambia.” Kisha Petro akawakaribisha ndani ya nyumba na kuwapangisha mule. Kesho yake Petro akafunga safari pamoja nao. Na wandugu waamini wamoja waliokaa Yopa wakamusindikiza. Kesho kutwa wakafika katika muji Kaisaria. Kornelio alikuwa akiwangojea pamoja na jamaa yake na warafiki zake aliowaalika. Petro alipokuwa akiingia ndani ya nyumba, Kornelio akaenda kumupokea, akapiga magoti mbele yake na kumwabudu. Lakini Petro akamwinua Kornelio na kumwambia: “Simama, kwa maana mimi ni mutu kama wewe.” Petro akaingia ndani ya nyumba akiwa akisimulia na Kornelio, na mule akakuta watu wengi wamekusanyika. Akawaambia: “Ninyi munajua wazi kama katika Sheria ya dini yetu inakatazwa kwa Muyuda kushirikiana na mutu wa taifa lingine wala kumutembelea. Lakini Mungu amenionyesha kwamba haifai kumuhesabia mutu yeyote kuwa muchafu wala mutengwa. Ni kwa sababu hii, wakati uliponitumia wajumbe, nilikuja pasipo kusita. Basi sasa ningependa kujua kwa sababu gani muliniita.” Kornelio akajibu: “Kumekwisha kupita siku tatu, mimi nilikuwa nikiomba ndani ya nyumba yangu kwa saa hii hii ya saa tisa ya muchana. Mara moja nikaona mutu anayevaa nguo yenye kungaa sana, akisimama mbele yangu. Naye akaniambia: ‘Kornelio, Mungu amesikia maombi yako na kukukumbuka kwa ajili ya misaada unayotoa kwa wamasikini. Basi tuma watu waende Yopa kwa kumwita mutu mumoja jina lake Simoni anayeitwa vilevile Petro. Naye anapanga kwa fundi mumoja anayetengeneza vitu vya ngozi anayeitwa Simoni. Nyumba yake iko pembeni ya bahari.’ Na pale pale nikatuma watu kwako, nawe umefanya vizuri kwa kufika. Sasa sisi wote tuko hapa mbele ya Mungu kwa kusikiliza mambo yote Bwana aliyokuagiza kutuambia.” Basi Petro akaanza kuhubiri, akisema: “Sasa ninafahamu kwamba Mungu hana upendeleo, lakini katika kila taifa mutu yeyote anayemutii Mungu na kutenda yanayokuwa ya haki, anamupendeza. Yeye ametuma ujumbe wake kwa Waisraeli, akiwahubiri Habari Njema ya amani kwa njia ya Yesu Kristo, anayekuwa Bwana wa watu wote. Ninyi munajua mambo yaliyotokea katika Yudea yote, yakianzia katika jimbo la Galilaya nyuma ya mahubiri ya Yoane yaliyoelekea ubatizo. Tena ninyi munajua namna Mungu alivyomuchagua Yesu wa Nazareti kwa kazi yake, akimujaza na Roho Mutakatifu na kumupatia uwezo. Naye alipita fasi zote akitenda mema na kuwaponyesha watu wote waliokuwa chini ya mamlaka ya Shetani. Ilitendeka vile kwa maana Mungu alikuwa pamoja naye. Na sisi tuko washuhuda wa mambo yote Yesu aliyofanya katika inchi ya Wayuda na katika muji wa Yerusalema. Walimwua kwa kumutundika juu ya musalaba, lakini Mungu akamufufua kwa siku ya tatu kisha kufa kwake na kumwonyesha waziwazi. Hakuonekana kwa watu wote, lakini kwa sisi tuliochaguliwa na Mungu kuwa washuhuda. Ni sisi tuliokula na kunywa pamoja naye nyuma ya kufufuka kwake. Akatuagiza kutangaza Habari Njema kwa watu na kushuhudia kwamba ni yeye aliyewekwa na Mungu kuwa Mwamuzi wa wazima na wafu. Manabii wote wanamushuhudia Yesu kwamba kila mutu anayemwamini atasamehewa zambi zake kwa uwezo wa jina lake.” Petro alipokuwa hajamaliza kusema maneno hayo, Roho Mutakatifu akashuka juu ya wote waliosikiliza mahubiri yake. Na wale wanafunzi Wayuda waliofika pamoja na Petro wakashangaa sana kwa kuona kwamba Mungu ametoa zawadi ya Roho wake Mutakatifu kwa watu wa mataifa mengine vilevile. Kwa maana waliwasikia wakisema kwa luga za ajabu na kumutukuza Mungu. Halafu Petro akasema: “Ni nani anayeweza kuwazuiza watu hawa waliopewa Roho Mutakatifu kama sisi wasibatizwe kwa maji?” Basi akaamuru wabatizwe kwa jina la Yesu Kristo. Na kisha wakamusihi Petro akae kule kwao kwa siku chache. Mitume na wandugu waamini waliokuwa Yudea wakasikia kwamba watu wamoja wa mataifa mengine wameamini Neno la Mungu vilevile. Na Petro aliporudi Yerusalema, wale wanafunzi Wayuda wakabishana naye, wakisema: “Uliingia ndani ya nyumba ya watu wasiokuwa wa taifa letu na kula chakula pamoja nao!” Halafu Petro akaanza kuwaelezea mambo yote yaliyotokea kwa utaratibu. Akawaambia: “Mimi nilikuwa katika muji Yopa nikiomba. Kisha nikakuwa sawa nimezimia, nami nikapata maono. Nikaona kitu kinachokuwa kama nguo kubwa kikishuka toka mbingu, kikitelemushwa, kikishikwa kwenye pembe zake ine. Nacho kikafika karibu nami. Nilipochungulia ndani yake kwa uangalifu, nikaona nyama wa ufugo wenye miguu mine, nyama wa pori, nao nyama wenye kutambaa pamoja na ndege. Na nikasikia sauti ikiniambia: ‘Petro, simama. Chinja na ukule!’ Lakini nikajibu: ‘Hapana, hata kidogo, ee Bwana! Ndani ya kinywa changu hamujaingia bado kitu chochote kisichoruhusiwa kukuliwa wala chochote kinachohesabiwa kuwa kichafu.’ Lakini sauti ikanirudilia kutoka mbingu ikisema: ‘Vitu vilivyotakaswa na Mungu, usivihesabu kuwa vichafu.’ Nayo maneno haya yakasikilika tena mara tatu, kisha vile vitu vyote vikanyanyuliwa mbinguni. Na saa ile ile watu watatu waliotumwa kwangu kutoka muji Kaisaria wakafika kwa mulango wa nyumba niliyokaa ndani yake. Naye Roho Mutakatifu akaniambia kwamba niende pamoja nao bila kusita. Na hawa wandugu sita munaowaona wakanisindikiza, nasi tukafika na kuingia sisi wote ndani ya nyumba ya Kornelio. Naye akatuelezea namna malaika alivyomutokea ndani ya nyumba yake na kumwambia: ‘Tuma wajumbe, kwenda Yopa kwa kumwita Simoni, anayeitwa vilevile Petro. Ni yeye atakayekuambia mambo yanayokupasa wewe pamoja na watu wote wa nyumba yako kusudi mupate kuokolewa.’ Nami nilipoanza kusema, Roho Mutakatifu akashuka juu yao sawa vile alivyoshuka juu yetu kwanza. Halafu nikakumbuka maneno haya Bwana aliyosema: ‘Yoane amebatiza kwa maji, lakini ninyi mutabatizwa kwa Roho Mutakatifu.’ Basi ikiwa Mungu aliwapa wale watu zawadi ile ile Roho Mutakatifu aliyotupatia sisi wakati tulipomwamini Bwana Yesu Kristo, mimi ni nani hata nisubutu kupingana na Mungu?” Wandugu waamini waliposikia maneno hayo, wakatulia na kumusifu Mungu, wakisema: “Kumbe Mungu amewajalia hata watu wa mataifa mengine vilevile kusudi waweze kugeuka toka zambi na kupata uzima kamili.” Nyuma ya kuuawa kwa Stefano, wanafunzi walisambaa kwa ajili ya mateso. Nao wakasafiri mpaka katika inchi ya Foinikia na ya Kipuro na kufika katika muji Antiokia. Na kule walihubiri Neno la Mungu, lakini kwa Wayuda peke yao tu. Lakini kulitokea wanafunzi wengine, waliokuwa watu wa Kipuro na wa inchi ya Kurene, waliofika Antiokia. Nao wakaanza kusemezana na Wagriki vilevile, wakiwahubiri Habari Njema juu ya Bwana Yesu. Na Bwana akawaongoza kwa uwezo wake, hata watu wengi sana wakaamini neno la Bwana na kumugeukia. Watu wa kanisa la Yerusalema waliposikia habari hii, wakamutuma Barnaba kwenda kule Antiokia. Naye alipofika, akaona mambo yote yaliyotendeka kutokana na neema ya Mungu, akafurahi, naye akawatia wanafunzi wote moyo kusudi waendelee kushikamana na Bwana kwa moyo wao wote. Barnaba alikuwa mutu mwema, mwenye kujazwa na Roho Mutakatifu na mwenye imani sana. Na watu wengi wakaongezeka kwa Bwana. Kisha Barnaba akatoka kule na kwenda Tarso kwa kumutafuta Saulo. Naye alipomwona, akamuleta Antiokia. Na kwa muda wa mwaka muzima Barnaba na Saulo walikusanyika katika kanisa la kule na wakawafundisha watu wengi. Ni kule Antiokia ndiko wanafunzi waliitwa kwa mara ya kwanza jina la Wakristo. Katika siku zile, manabii wamoja walifika Antiokia wakitoka Yerusalema. Na mumoja wao, aliyeitwa Agabo, akasimama, akatabiri kwa njia ya Roho Mutakatifu kwamba kutakuwa njaa kubwa katika dunia nzima. (Nayo ikatokea katika nyakati za utawala wa mufalme Klaudio wa Roma.) Wanafunzi wakakusudia kutuma musaada kwa wandugu waamini waliokaa katika jimbo la Yudea, kila mumoja kwa kadiri alivyoweza kutoa. Nao wakafanya vile, wakatuma misaada waliyokusanya kwa wazee wa kanisa kwa mukono wa Barnaba na Saulo. Katika siku zile mufalme Herode akaanza kutesa watu wamoja wa kanisa. Akaamuru Yakobo, ndugu ya Yoane, auawe kwa upanga. Basi, alipoona kwamba jambo lile liliwapendeza Wayuda, akaamuru Petro afungwe vilevile. (Mambo haya yalitokea kwa wakati wa sikukuu ya Mukate Usiotiwa Chachu.) Alipokwisha kumukamata Petro, na kumutia katika kifungo, akamuweka chini ya ulinzi wa vikundi vine vya waaskari waliogomboana wane kwa wane. Naye alikusudia kumusambisha mbele ya watu nyuma ya sikukuu ya Pasaka. Basi Petro akabaki akichungwa katika kifungo, lakini kanisa likaendelea kumwombea kwa Mungu pasipo kuchoka. Usiku, mbele ya kutimia kwa siku Herode aliyotaka kumusambisha mbele ya watu, Petro alikuwa amelala ndani ya chumba katikati ya waaskari wawili. Alikuwa amefungwa na minyororo miwili, nao walinzi walikuwa wakichunga mulango wa kifungo. Kwa rafla malaika wa Bwana akatokea na mwangaza ukajaa ndani ya chumba kile. Malaika akamutikisa Petro na kumwamusha, akimwambia: “Simama upesi!” Nayo minyororo ikaanguka toka kwenye mikono yake. Kisha malaika akamwambia: “Funga mukaba na uvae viatu vyako.” Petro akafanya vile, naye malaika akamwambia tena: “Vaa koti yako na kunifuata.” Petro akamufuata mpaka inje ya kifungo. Lakini hakutambua kwamba mambo yale malaika aliyofanya yalikuwa ya kweli; alizani kwamba amepata maono. Wakapita kikundi cha kwanza cha waaskari na cha pili, na kufikia kwenye mulango wa chuma wa kuingilia ndani ya muji. Ule mulango ukajifungua wenyewe mbele yao, nao wakatoka inje na kuendelea katika barabara moja. Na kwa rafla yule malaika akamwacha. Petro alipotambua kwamba mambo yaliyotokea ni ya kweli akasema: “Sasa ninajua hakika kwamba Bwana alimutuma malaika wake kuniokoa katika mikono ya Herode na katika mabaya yote Wayuda waliotaka kunitendea.” Alipokwisha kufahamu mambo yale yaliyotokea, akaenda kwa Maria, mama ya Yoane aliyeitwa Marko. Watu wengi walikuwa wamekusanyika mule, wakiomba. Petro alipiga hodi kwenye mulango wa inje, mujakazi mumoja aliyeitwa Roda akakuja kwenye mulango. Naye akatambua sauti ya Petro akafurahi sana hata kwa pahali pa kufungua mulango akarudi mbio kuwapasha wengine kwamba Petro anasimama mbele ya mulango. Nao wakamwambia: “Uko na wazimu!” Lakini akakaza kusema kwamba ni kweli. Basi wakasema: “Ni malaika wake.” Kwa wakati ule Petro akaendelea tu kupiga hodi. Walipofungua mulango wakamwona, na kushangaa. Naye akawanyamazisha kwa kunyoosha mukono, kuwaelezea namna Bwana alivyomwondoa katika kifungo. Akawaambia tena: “Muwaelezee Yakobo na wandugu wengine waamini habari hizi.” Kisha Petro akaondoka na kwenda nafasi ingine. Kulipokucha, waaskari wakapigwa na hofu sana. Wakaanza kuulizana: “Jambo gani lililomupata Petro?” Herode akaomba wamutafute, lakini hawakumwona. Kwa hiyo kisha kusambisha wale walinzi, akaamuru wauawe. Halafu Herode akaondoka Yudea kwenda katika muji Kaisaria na kukaa kule kwa muda. Herode alikuwa amechunga hasira sana juu ya watu wa muji Tiro na wa Sidona. Lakini wakapatana kwa nia moja kwa kumwendea. Kwanza wakasikilizana na Balasto, aliyekuwa musimamizi wa nyumba ya mufalme. Kisha wakaomba mapatano ya amani kwa mufalme Herode, kwa sababu inchi yao ilitegemea inchi ya mufalme huyo kwa kupata chakula. Halafu kwa siku ile iliyopangwa, Herode akavaa nguo zake za kifalme, akaikaa katika kiti chake cha kifalme na kuwatolea watu hotuba. Nao watu wakalalamika wakisema: “Hii ni sauti ya Mungu, wala si ya mutu.” Na pale pale malaika wa Bwana akamwazibu Herode kwa ugonjwa kwa sababu alijitukuza kwa pahali pa Mungu. Herode akakuliwa na michango ya tumbo na kisha akakufa. Lakini Neno la Mungu likaendelea mbele na kuenea fasi nyingi. Barnaba na Saulo walipomaliza kazi yao, wakarudi toka Yerusalema, wakiwa pamoja na Yoane, aliyeitwa vilevile Marko. Katika kanisa la Antiokia kulikuwa manabii na walimu wamoja. Kati yao kulikuwa Barnaba, Simoni aliyeitwa vilevile Nigeri; Lukio wa Kurene, Saulo na Manaeni, aliyekomaa pamoja na mufalme Herode. Siku moja walipokuwa wakifanya ibada, wakiwa wamefunga kula chakula, Roho Mutakatifu akasema: “Muwasimike Barnaba na Saulo kwa kazi ile niliyowachagulia.” Basi wakafunga tena kula chakula na kuomba. Kisha wakaweka mikono juu yao na kuwatuma waende safari. Halafu Barnaba na Saulo wakaenda kwenye kivuko cha Seleukia kwa uongozi wa Roho Mutakatifu. Kule wakaingia ndani ya chombo na kwenda mpaka katika kisanga cha Kipuro. Nao walipofika katika muji Salami, wakahubiri Neno la Mungu katika nyumba za kuabudia za Wayuda. Yoane alikuwa pamoja nao, akiwasaidia kwa kufanya kazi. Walipokwisha kupita katika kisanga chote, wakafika katika muji Pafo. Kule wakakutana na Muyuda mumoja aliyekuwa muchawi na nabii wa uongo, jina lake Bara-Yesu. Huyo alitumika pamoja na liwali mumoja mwenye akili, aliyeitwa Sergio Paulo. Liwali huyo akawaita Barnaba na Saulo wafike kwake kwa sababu alitaka kusikia Neno la Mungu. Lakini yule muchawi Elema, (kufuatana na maana ya jina lake katika Kigriki), akapingana nao, akitaka kumugeuza yule liwali kusudi asiamini Neno la Mungu. Halafu Saulo, anayeitwa vilevile Paulo, akiwa amejazwa na Roho Mutakatifu, akamukazia macho na kusema: “Wewe mutoto wa Shetani unayejaa udanganyifu na ukorofi wa kila namna! Wewe usiyependa kuona jambo la haki! Wewe hauchoki na kugeuza maneno ya ukweli ya Bwana! Basi, sasa Bwana atakuazibu, nawe utakuwa kipofu, wala hautaweza hata kidogo kuona mwangaza kwa muda.” Mara moja macho ya Elema yakaingiwa na giza hata yakapofuka, naye akaanza kupapasapapasa akitafuta mutu wa kumwongoza. Yule liwali alipoona mambo yale yaliyotokea, akashangaa na mafundisho ya Bwana hata akapata kumwamini. Kisha Paulo na wenzake wakaingia ndani ya chombo, wakaondoka katika muji Pafo na kwenda katika muji Perga katika jimbo la Pamfilia. Walipofika kule Yoane aliyeitwa vilevile Marko akaachana nao na kurudi Yerusalema. Kutoka kule wakaendelea na safari yao na kufika mpaka katika muji Antiokia wa jimbo la Pisidia. Siku ya Sabato ilipotimia, wakaingia ndani ya nyumba ya kuabudia na kuikaa mule. Na nyuma ya kusoma katika vitabu vya Sheria na vya manabii, wakubwa wa ile nyumba ya kuabudia wakatuma mutu kwa kuwaambia: “Wandugu, ikiwa muko na maneno ya kuwatia watu moyo, muyaseme.” Basi Paulo akasimama, akainua mukono kwa kuwaalika wanyamaze. Akasema: “Munisikilize ninyi wanainchi wenzangu Waisraeli, nanyi watu wa mataifa mengine munaomwogopa Mungu! Mungu wa taifa hili la Waisraeli aliwachagua babu zetu, naye akawafanya kuwa taifa kubwa walipokuwa wakikaa kama wageni katika inchi ya Misri. Kisha akawaondosha kule kwa uwezo wake mukubwa na kuwavumilia katika jangwa kwa muda wa miaka makumi ine. Naye alipokwisha kuteketeza mataifa saba yaliyokaa katika inchi ya Kanana, akatoa inchi ile kwa lile taifa lake kuwa urizi wao. Mambo haya yote yalitendeka kwa muda wa miaka yapata mia ine makumi tano. “Kisha akawapa waamuzi kwa kuwaongoza mpaka katika siku za nabii Samweli. Na kisha wakaomba wapewe mufalme. Kwa hiyo Mungu akawawekea Saulo, mwana wa Kisi, wa kabila la Benjamina kwa kuwatawala kwa muda wa miaka makumi ine. Kisha kumwondosha Saulo, Mungu akasimika Daudi kuwa mufalme wao. Na yeye mwenyewe alimushuhudia akisema: ‘Nimejichagulia Daudi mwana wa Yese, kwa maana ni mutu mwenye kunipendeza. Huyu ndiye atakayefanya mambo yote ninayotaka.’ Na toka katika uzao wa mutu huyo Mungu akawaletea Waisraeli Mwokozi, ndiye Kristo, kama vile alivyokuwa amewaahidia. Mbele Yesu hajajionyesha, Yoane alihubiri kwa Waisraeli wote kwamba wageuke toka zambi zao na kubatizwa. Na Yoane alipokaribia kwa mwisho wa kazi yake, alisema: ‘Munafikiri mimi ni nani? Mimi siko yule munayengojea. Lakini angalia, nyuma yangu kutakuja mutu ambaye mimi sistahili hata kufungua kamba za viatu vyake.’ “Wandugu zangu, ninyi wazao wa Abrahamu na ninyi watu wa mataifa mengine munaokuwa hapa kwa kumwabudu Mungu, habari hii ya wokovu imetumwa kwetu! Wakaaji wa Yerusalema na wakubwa wao hawakumutambua Yesu wala maandiko ya manabii yaliyosomwa kila siku ya Sabato. Lakini ingawa hivi wakatimiza maandiko yale kwa njia ya kumuhukumu kufa. Ijapokuwa hawakupata sababu ya kumuhukumu kufa, wakamwomba Pilato awape ruhusa ya kumwua. Na wakati walipokwisha kutimiza yote yaliyoandikwa juu yake, wakamushusha toka juu ya musalaba na kumuzika. Lakini Mungu akamufufua. Na kwa siku nyingi akaonekana kwa waliosafiri pamoja naye toka Galilaya kwenda Yerusalema. Na wale ndio sasa wanaomushuhudia mbele ya watu. Na sasa sisi tunahubiri Habari Njema kwenu kwamba, ile Mungu aliyoitoa kwa babu zetu ameitimiza kwa ajili yetu sisi wazao wao. Amefanya hivi kwa kumufufua Yesu kwa kuhakikisha maandiko haya ya Zaburi ya pili yanayosema: ‘Wewe ni mwana wangu, mimi leo ninakuwa baba yako.’ Na juu ya ufufuko wa Yesu, kusudi asipate kuoza, Mungu alisema: ‘Nitakupa baraka takatifu zinazokuwa za hakika, nilizomwahidia Daudi.’ Na kwa hiyo inasemwa tena katika maandiko mengine: ‘Hautakubali mutumishi wako mutakatifu aoze.’ Lakini Daudi alipokwisha kutumika sawasawa na kusudi la Mungu katika maisha yake, akakufa na kwenda kukutana na babu zake waliomutangulia, naye akaoza. Lakini yule Mungu aliyemufufua hakuoza. Basi mujiangalie vizuri kusudi maneno haya ya manabii yasiwapate ninyi: ‘Muangalie, ninyi wenye kuzarau, mupigwe na mushangao na mutoweke! Maana katika siku hizi nitafanya jambo ambalo ninyi musingeweza kusadikia hata wangewaelezea.’ ” Paulo na Barnaba walipotoka ndani ya ile nyumba ya kuabudia, watu wakawasihi warudie tena kuwaelezea maneno yale yale kwa siku ya Sabato iliyofuata. Nyuma ya mukutano, Wayuda wengi na watu wa mataifa mengine waliogeuka kufuata dini ya Kiyuda, waliomwogopa Mungu, wakawafuata Paulo na Barnaba. Nao wawili wakasema na watu hao na kuwatia moyo kusudi waendelee kutegemea neema ya Mungu. Siku ya Sabato iliyofuata, karibu watu wote wa muji wakakusanyika kwa kusikia neno la Bwana. Wayuda walipoona lile kundi la watu, wakajaa na wivu sana, nao wakapinga maneno Paulo aliyosema na kumutukana. Halafu Paulo na Barnaba wakawaambia bila woga: “Ilitupasa kwanza kuhubiri Neno la Mungu kwenu. Lakini kwa kuona mumelikataa na kujihesabu ninyi wenyewe kwamba uzima wa milele haufai kwenu, basi tunashugulika na watu wa mataifa mengine. Kwa maana Bwana ametuagiza hivi: ‘Nimekuweka kuwa mwangaza wa mataifa, kusudi watu wapate kuokolewa katika dunia yote.’ ” Wakati watu wa mataifa mengine waliposikia maneno haya wakafurahi, wakatukuza neno la Bwana. Nao wote waliokuwa wamechaguliwa kwa kupata uzima wa milele, wakaamini. Neno la Bwana likaenea katika inchi ile yote. Lakini Wayuda wakawashawishi wakubwa wa muji pamoja na wanawake wamoja wenye heshima, walioabudu Mungu. Wakawatesa Paulo na Barnaba hata wakawafukuza toka katika inchi yao. Halafu hawa mitume wakawakungutia mavumbi toka juu ya miguu yao, na kwenda katika muji Ikonio. Nao wanafunzi wa Antiokia walijazwa na furaha na Roho Mutakatifu. Paulo na Barnaba walipofika katika muji Ikonio, wakaingia vilevile katika nyumba ya kuabudia ya Wayuda. Mule wakahubiri hata kundi kubwa la Wayuda na mataifa mengine wakaamini. Lakini Wayuda waliokataa kuamini walishawishi watu wa mataifa mengine na kuwasukuma kuwachukia wandugu waamini. Paulo na Barnaba wakakaa Ikonio kwa muda murefu. Walisema kwa uhodari kabisa, wakimutumainia Bwana. Naye aliwapa uwezo wa kufanya maajabu na vitambulisho. Na kwa njia hiyo alihakikisha kwamba ujumbe walioutangaza juu ya neema yake ulikuwa wa kweli. Watu wa muji wakatengana: wamoja walikuwa upande wa Wayuda na wengine upande wa mitume. Kisha Wayuda wamoja na watu wa mataifa mengine pamoja na wakubwa wao, wakakusudia kuwatendea mitume vibaya na kuwaua kwa kuwatupia mawe. Paulo na Barnaba walipotambua jambo lile wakakimbilia katika muji wa Listra na wa Derbe ndani ya wilaya ya Likaonia na katika sehemu za kandokando yake. Kule wakaendelea kuhubiri Habari Njema. Kule Listra kulikuwa mutu mumoja aliyekuwa kiwete tangia kuzaliwa. Yeye hakuweza kusimama wala kupima kutembea. Yeye alikuwa akisikiliza mahubiri ya Paulo. Paulo akamukazia macho, naye akaona kwamba kiwete yule yuko na imani ya kuweza kuponyeshwa. Halafu akamwambia kwa sauti: “Simama wima!” Mutu yule akaruka akasimama na kuanza kutembea. Wakati makundi ya watu walipoona jambo lile Paulo alilofanya, wakasema kwa sauti katika luga yao ya kilikaonia: “Miungu imetushukia ikiwa na sura ya kimutu!” Walimupanga Barnaba jina la mungu Zeu, na Paulo jina la mungu Herme, kwa sababu yeye ndiye aliyetoa hotuba. Naye kuhani wa hekalu la mungu Zeu, lililokuwa kwenye kiingilio cha muji, akaleta ngombe waliopambwa na mafungu za maua mbele ya mulango. Maana yeye pamoja na kundi la watu walitaka kuwatolea wale mitume sadaka ya nyama wenye kuchinjwa. Lakini Barnaba na Paulo waliposikia habari ile, wakapasua nguo zao kwa huzuni, wakaingia haraka katikati ya kundi la watu, na kusema kwa sauti: “Wandugu, kwa sababu gani munafanya mambo kama haya? Sisi vilevile ni watu, tuko sawasawa nanyi, na tunawahubiri ninyi Habari Njema kwamba muache kuabudu vitu hivi vya bure na mumugeukie Mungu mwenye uzima; yeye aliyeumba mbingu na dunia, bahari na vyote vinavyokuwa ndani yao. Katika siku zilizopita Mungu aliwaachilia watu wa mataifa yote wafuate njia wanazotaka. Ingawa vile hakuacha kujijulisha kwa njia ya kutenda mema. Anawanyeshea mvua toka mbingu, anawapa mavuno kwa wakati wake, anawapa chakula na kuwajaza na furaha.” Ijapokuwa mitume walisema maneno haya, ilikuwa vigumu kuzuiza makundi ya watu wasiwatolee sadaka. Kisha Wayuda wamoja wakakuja tokea katika muji wa Antiokia na wa Ikonio. Wakashawishi makundi ya watu wajiunge nao. Wakamutupia Paulo mawe na kumukokotea inje ya muji, wakizani kwamba amekwisha kufa. Lakini wanafunzi walipokuwa wakimuzunguka, akasimama na kurudi ndani ya muji. Kesho yake yeye pamoja na Barnaba wakaenda katika muji wa Derbe. Paulo na Barnaba walihubiri Habari Njema katika muji wa Derbe, na kupata wanafunzi wengi. Kisha wakarudi katika muji wa Listra, wa Ikonio na wa Antiokia ya Pisidia. Kule waliwajenga wanafunzi moyo na kuwatia nguvu wabakie katika imani wakiwaambia: “Ni sherti tupite katika mateso mengi kwa kuweza kuingia katika Ufalme wa Mungu.” Wakawachagua wazee katika kila kanisa. Na kisha kuomba na kufunga kula chakula, wakawaweka chini ya ulinzi wa Bwana waliyemwamini. Kisha wakapitia katika jimbo la Pisidia na kufika katika inchi ya Pamfilia. Walipokwisha kuhubiri Neno la Mungu kwa watu wa muji Perga, wakaenda katika muji wa Atalia. Na kutoka kule wakarudi mpaka Antiokia kwa njia ya chombo. Ni kule walipokuwa wameombewa neema kwa Mungu kwa ajili ya kazi ile waliyotoka kutimiza. Walipofika Antiokia, wakafanya mukutano wa kanisa na kuwaelezea mambo yote Mungu aliyofanya kwa njia yao, na namna alivyowafungulia watu wa mataifa mengine mulango kusudi wao vilevile wapate kuamini. Nao wakakaa kule Antiokia kwa muda wa siku nyingi pamoja na wanafunzi. Watu wamoja walishuka toka Yudea kwenda Antiokia, nao wakaanza kuwafundisha wandugu waamini kwamba hawawezi kuokoka ikiwa hawatahiriwi sawa vile inavyoagizwa katika Sheria ya Musa. Basi Paulo na Barnaba wakapingana na kubishana nao vikali sana juu ya jambo hili. Na kwa hiyo wandugu waamini wakaagiza Paulo na Barnaba pamoja na watu wengine kati yao waende Yerusalema kusemezana na mitume na wazee wa kanisa la kule juu ya maneno yale. Kanisa liliwapatia vitu walivyohitaji kwa ajili ya safari ile, nao wakapita katika inchi ya Foinikia na katika Samaria. Na kule wakaeleza namna watu wa mataifa mengine walivyomugeukia Mungu. Habari hii ikafurahisha sana wandugu waamini wote. Walipofika Yerusalema, wakakaribishwa na kanisa pamoja na mitume na wazee, nao wakawaelezea mambo yote Mungu aliyofanya kwa njia yao. Lakini wanafunzi wamoja waliokuwa katika chama cha Wafarisayo wakasimama na kusema: “Sherti watu wa mataifa mengine walioamini watahiriwe na kuagizwa wafuate Sheria ya Musa.” Halafu mitume na wazee wa kanisa wakakusanyika kusudi wachunguze neno hili. Mabishano yalipoendelea, Petro akasimama na kusema: “Wandugu zangu, munajua kwamba Mungu alinichagua pale zamani kati yenu kusudi nihubiri Habari Njema kwa watu wa mataifa mengine wapate kuisikia na kuamini. Naye Mungu anayejua mafikiri ya mutu, alihakikisha kwamba amewakubali watu wa mataifa mengine kwa njia ya kuwapatia Roho Mutakatifu sawa vile alivyotupatia sisi. Yeye hakufanya ubaguzi kati yetu na wao; ametakasa mioyo yao kwa sababu walimwamini. Basi sasa, kwa nini munataka kumupima Mungu kwa kuwabebesha muzigo ambao wala babu zetu, wala sisi wenyewe hatukuweza kuubeba? Haipaswi kuwa vile, kwa maana sisi na wao vilevile tunaamini kwamba sisi wote tunaokolewa kwa neema ya Bwana Yesu.” Basi mukutano wote ukabaki kimya ukisikiliza maelezo ya Barnaba na Paulo juu ya vitambulisho na maajabu yote Mungu aliyofanya kwa njia yao katikati ya watu wa mataifa mengine. Nao walipomaliza kusema, Yakobo akajibu, akisema: “Wandugu zangu, munisikilize! Simoni anatoka kutuelezea namna Mungu alivyowashugulikia watu wa mataifa mengine pale mbele kusudi ajichagulie wamoja kati yao kuwa watu wake wa pekee. Na jambo hilo linapatana na maneno haya ya manabii yaliyoandikwa katika Maandiko Matakatifu: ‘Nyuma ya mambo haya nitarudi, nitaimarisha tena ufalme wa Daudi, nitausimamisha tena sawa wanavyojenga tena nyumba iliyoanguka, kusudi watu wote wengine wamugeukie Bwana, watu wa mataifa yote wapate kuwa watu wangu wa pekee. Ni vile Bwana anavyosema, yeye aliyejulisha mambo haya tangu zamani za kale.’ ” Yakobo akaendelea kusema: “Ni kwa sababu hii, mimi ninaona kwamba haifai tuwasumbue watu wa mataifa mengine wanaomugeukia Mungu. Lakini inafaa tuwaandikie kwa kuwaambia kwamba wajitenge na vitu vilivyochafuliwa kwa kutambikia sanamu, waepuke uasherati na wasikule nyamafu wala damu. Kwa maana tangu zamani Sheria ya Musa inasomwa kila siku ya Sabato katika nyumba za kuabudia na kuhubiriwa katika kila muji.” Halafu mitume na wazee wakakata shauri pamoja na kanisa lote la Yerusalema kwamba wachague watu wamoja kati yao na kuwatuma kwenda Antiokia pamoja na Paulo na Barnaba. Wakachagua Yuda aliyeitwa vilevile Barisaba, pamoja na Sila. Watu hawa wawili walihesabiwa na wandugu waamini kuwa wenye heshima sana. Nao wakawatuma na barua iliyoandikwa hivi: “Sisi mitume na wazee wa kanisa na wandugu zenu, tunawasalimu ninyi wandugu zetu waamini wa mataifa mengine munaokuwa katika muji wa Antiokia na katika jimbo la Suria na la Kilikia. Tumesikia kwamba watu fulani waliotoka huku kwetu pasipo ruhusa yetu wamewasumbua ninyi na maneno na kuwatia katika wasiwasi. Kwa sababu hii sisi tumekata shauri kwa nia moja, tukapatana kuchagua watu wamoja na kuwatuma kwenu. Watu hawa watawafikia pamoja na wapendwa wetu, Barnaba na Paulo, waliotoa maisha yao kwa ajili ya kumutumikia Bwana wetu Yesu Kristo. Ni hivi tunawatuma kwenu Yuda na Sila, nao watawaelezea waziwazi kwa kinywa maneno haya tunayowaandikia. Kwa maana kutokana na shauri la Roho Mutakatifu na shauri letu wenyewe tumeamua kwamba hatutawabebesha muzigo mwingine muzito kupita mapaswa haya ya lazima: musikule vyakula vilivyotolewa kwa kutambikia sanamu; musikule damu wala nyamafu; na muepuke uasherati. Mutafanya vema kama mukijitenga na mambo haya. Salamu kwenu.” Kisha kuagana, wale wajumbe wakaondoka na kwenda Antiokia. Kule wakakusanya kundi lote la waamini, wakawapa barua ile. Nao walipoisoma wakafurahi kwa ajili ya maneno ya kuwatia moyo yaliyoandikwa ndani yake. Na kufuatana na vile Yuda na Sila walivyokuwa manabii, wakawaonya kwa maneno mengi na kuwajenga moyo. Kisha kukaa kule kwa muda, wandugu waamini wakawaaga na kuwatakia amani wakawaruhusu kurudi kwa wale waliowatuma. [ Lakini Sila akaona vizuri kubakia kule.] Naye Paulo na Barnaba wakabakia Antiokia, na kule wao pamoja na watu wengine wengi walifundisha na kuhubiri neno la Bwana. Nyuma ya siku chache, Paulo akamwambia Barnaba: “Turudi sasa kwa kuwaangalia wandugu waamini katika miji ambamo tulihubiri neno la Bwana, kusudi tuone kama wako katika hali gani.” Barnaba alitaka waende pamoja na Yoane, aliyeitwa vilevile Marko. Lakini Paulo hakuona vizuri kwenda naye kwa sababu alikuwa ameachana nao katika inchi ya Pamfilia, akikataa kuendelea nao katika kazi. Kwa hiyo Paulo na Barnaba wakabishana vikali hata wakatengana. Barnaba akaondoka pamoja na Marko, wakaingia ndani ya chombo na kwenda katika kisanga cha Kipuro. Naye Paulo akachagua kwenda na Sila, nao wandugu waamini walipokwisha kuwaombea neema kwa Mungu, wakaondoka. Akapita katika jimbo la Suria na Kilikia, na kule akayatia makanisa nguvu. Paulo akafika Derbe na Listra, ambako kulikuwa mwanafunzi mumoja aliyeitwa Timoteo. Mama yake alikuwa Muyuda, naye alikuwa ameamini lakini baba yake alikuwa Mugriki. Nao wandugu waamini wa Listra na wa muji Ikonio walitoa ushuhuda muzuri juu ya Timoteo. Paulo alitaka Timoteo amusindikize katika safari zake. Kwa hiyo akamutahiri kwa sababu ya Wayuda waliokaa katika pande zile, kwa maana wote walijua kwamba baba yake alikuwa Mugriki. Na katika miji yote ambamo walipita walitangaza kwa wanafunzi yale maagizo yaliyotolewa na mitume na wazee wa kanisa la Yerusalema, wakiwaomba wayashike. Hivi makanisa yakaendelea kukomaa katika imani, nayo hesabu ya wanafunzi iliongezeka siku kwa siku. Paulo na wale waliomusindikiza wakapita katika inchi ya Furigia na ya Galatia kwa sababu Roho Mutakatifu alikuwa amewakataza wasihubiri Neno la Mungu katika jimbo la Azia. Nao walipofika katika wilaya ya Misia, wakajaribu kwenda katika jimbo la Bitinia, lakini Roho wa Yesu hakuwaruhusu. Kwa hiyo wakapita Misia, wakatelemuka mpaka wakafika katika muji Troa. Na ilipokuwa usiku akapata maono. Akaona mutu mumoja wa inchi ya Makedonia akisimama mbele yake akimusihi akisema: “Vuka, ufike kwetu Makedonia, utusaidie.” Na pale pale kisha kupata maono yale, tukajitayarisha kwenda Makedonia, kwa maana tulitambua hakika kwamba Mungu alituita kwenda kuhubiri Habari Njema kule. Basi tukasafiri ndani ya chombo kutoka Troa na kwenda mara moja mpaka Samotirake, na kesho yake tukafika Neapoli. Kutoka kule tukafika mpaka Filipi, muji mukubwa wa inchi ya Makedonia uliokuwa chini ya utawala wa Waroma. Nasi tukakaa katika muji ule kwa muda wa siku chache. Siku ya Sabato ilipotimia tukatoka ndani ya muji ule na kwenda karibu na muto mumoja, kwenye nafasi tulipozania kuwa ya kufanyia maombi. Tukaikaa na kusemezana na wanawake waliokusanyika pale. Na kati ya wanawake wale kulikuwa mwanamuke mumoja aliyeitwa Ludia, wa muji Tuatera. Yeye alikuwa muchuuzi wa nguo nyekundu za bei kali na mwenye kuogopa Mungu. Mwanamuke yule akatusikiliza kwa maana Bwana alimufungua moyo kusudi apate kufuata kabisa maneno Paulo aliyosema. Kisha yeye na watu wa nyumba yake wakabatizwa. Naye akatusihi akisema: “Ikiwa munakubali kweli kwamba ninamwamini Bwana, basi mufike mupange ndani ya nyumba yangu.” Akatulazimisha tuitike. Siku moja tulipokuwa tukienda kule kwenye nafasi ya kufanyia maombi, tukakutana na mujakazi mumoja. Yule mwanamuke alikuwa na pepo wa kuaguza ndani yake. Na kwa njia ya uaguzi ule aliwatajirisha wabwana wake. Mwanamuke yule akaendelea kumufuata Paulo na sisi, akilalamika akisema: “Watu hawa ni watumishi wa Mungu Mukubwa. Wanawatangazia ninyi namna gani munavyoweza kuokolewa.” Naye akafanya hivi kwa muda wa siku nyingi. Na kwa mwisho Paulo akachukizwa naye. Basi akageuka na kumwambia yule pepo: “Ninakuamuru kwa jina la Yesu Kristo, utoke ndani yake!” Na saa ile ile yule pepo akatoka ndani yake. Halafu wabwana wa yule mujakazi wakaona kwamba hawataweza tena kupata mali kutoka kwa yule aliyekuwa kitumaini chao. Kwa hiyo wakakamata Paulo na Sila, wakawakokota na kuwapeleka mbele ya wakubwa kwenye nafasi ya makutano. Walipowafikisha kwa watawala wa Waroma, wakasema: “Watu hawa ni Wayuda, nao wanaleta fujo katika muji wetu. Wanafundisha desturi ambazo sisi Waroma tunakatazwa kukubali na kufuata.” Basi kundi la watu waliokuwa pale wakawashambulia Paulo na Sila, nao watawala wakaamuru wawavue nguo kwa kinguvu na kuwapiga fimbo. Walipokwisha kuwapiga sana, wakawatia ndani ya kifungo na kumwagiza mulinzi wa kifungo awachunge kabisa. Na kufuatana na agizo lile, akawatia katika chumba cha ndani kabisa na kuwafungia miguu juu ya vipande vya miti kusudi ibaki imepanuka. Na katikati ya usiku, Paulo na Sila walikuwa wakimwomba Mungu na kumwimbia nyimbo za sifa, nao wafungwa wengine walikuwa wakiwasikiliza. Kwa rafla kukatokea tetemeko kubwa la inchi hata misingi ya nyumba ya kifungo ikatikisika. Na pale pale milango yote ikafunguka na minyororo ya wafungwa wote ikakatika. Mulinzi akaamuka, naye alipoona kwamba milango ilikuwa wazi, akachomoa upanga wake kusudi ajiue, kwa sababu aliwaza kama wafungwa wametoroka. Lakini Paulo akalalamika kwa nguvu akisema: “Usijiue, kwa maana sisi wote tuko hapa!” Basi yule mulinzi akaomba wamuletee taa, akarukia mbio ndani, akajitupa mbele ya Paulo na Sila, akitetemeka kwa hofu. Kisha akawapeleka inje na kuwauliza: “Wabwana wangu, inanipasa kufanya nini kusudi nipate kuokolewa!” Nao wakajibu: “Umwamini Bwana Yesu, nawe utaokolewa pamoja na watu wote wa nyumba yako.” Halafu wakamwelezea neno la Bwana pamoja na watu wote wa nyumba yake. Saa ile ile ya usiku mulinzi wa kifungo akawatwaa na kuwasafisha vidonda, naye akabatizwa pale pale na watu wake wote. Kisha akapeleka Paulo na Sila ndani ya nyumba yake na kuwapatia chakula. Yeye pamoja na watu wote wa nyumba yake walifurahi sana kwa sababu wamemwamini Mungu. Na kesho yake kulipokucha, watawala wakatuma watumishi wamoja kwa yule mulinzi wa kifungo kwa kumwambia: “Uwafungue wale watu.” Yule mulinzi wa kifungo akamwelezea Paulo habari ile akimwambia: “Wakubwa wametuma habari kwamba mufunguliwe. Basi sasa mutoke na kujiendea na amani.” Lakini Paulo akawaambia wajumbe: “Wametupiga mbele ya watu wote bila kutusambisha, ijapokuwa sisi ni wanainchi wa Roma, na kisha wakatutia ndani ya kifungo. Na sasa namna gani wanataka kututosha kwa uficho? Haiwezekani! Wao wenyewe wafike kutufungua!” Wale wajumbe wakarudi na kuwapasha wakubwa maneno yale. Nao waliposikia kwamba Paulo na Sila ni wanainchi wa Roma, wakaogopa sana. Basi wakakuja, wakawabembeleza, wakawapeleka inje ya kifungo na kuwasihi watoke katika muji ule. Paulo na Sila walipotoka ndani ya kifungo, wakaenda kwa Ludia. Nao walipokwisha kuonana na wandugu na kuwatia moyo, wakaondoka. Wakaendelea na safari yao, wakapita katika muji wa Amfipoli na wa Apolonia, na wakafika Tesalonika. Kule kulikuwa nyumba ya kuabudia ya Wayuda. Na sawa ilivyokuwa desturi, Paulo akaingia katika nyumba ile. Kwa muda wa siku tatu za Sabato zilizofuatana juma kwa juma, akabishana na watu waliokuwa mule, akitumia Maandiko Matakatifu. Aliwaelezea na kuwaonyesha wazi kwamba Kristo alipaswa kuteswa na kufufuka. Akawaambia: “Huyu Yesu ninayemuhubiri kwenu ndiye Kristo.” Wamoja kati ya Wayuda wakasadiki na kujiunga pamoja na Paulo na Sila. Vilevile kundi kubwa la Wagriki walioogopa Mungu pamoja na wanawake wengi wenye heshima wakasadiki. Lakini Wayuda wakajaa na wivu, hata wakakusanya watu wamoja wa ovyo ovyo waliowakuta kwenye nafasi za makutano, na kufanya kikundi. Kisha wakafanya fujo katika muji wote. Wakashambulia nyumba ya Yasoni, wakiwatafuta Paulo na Sila kusudi wawapeleke mbele ya watu. Kwa kuwa hawakuwapata, wakamupeleka Yasoni pamoja na wandugu waamini wengine mbele ya wakubwa wa muji. Wakalalamika wakisema: “Watu hawa walifanya fujo fasi zote na sasa wamefika huku. Naye Yasoni amewakaribisha kwake! Hawa wote wanatembea kinyume cha amri za Mufalme wa Roma wakisema kwamba kuna mufalme mwingine anayeitwa Yesu.” Maneno haya yakafazahisha kundi la watu pamoja na wakubwa wa muji. Wakubwa wa muji walipokwisha kumulipisha Yasoni na wenzake feza, wakawaachilia kwenda. Mara moja ilipokuwa usiku, wanafunzi wakawasindikiza Paulo na Sila waende Beroya. Nao walipofika kule, pale pale wakaingia katika nyumba ya kuabudia ya Wayuda. Watu hao walikuwa wenye nia nzuri zaidi kuliko watu wa Tesalonika; nao walipokea Neno la Mungu kwa hamu kubwa. Kila siku walichunguza Maandiko Matakatifu wapate kujua kwamba maneno Paulo aliyosema yalikuwa ya haki. Basi Wayuda wengi kati yao wakaamini pamoja na wanawake wengi Wagriki wenye heshima, na hesabu yenye kutosha ya wanaume vilevile. Lakini Wayuda wa muji wa Tesalonika wakapata habari kwamba Paulo anahubiri Neno la Mungu vilevile katika muji Beroya. Kwa hiyo wakaenda kule, wakaanza kufanya fujo kati ya makundi ya watu na kuwachochea. Halafu pale pale, wandugu waamini wakamusindikiza Paulo mpaka kwenye kivuko, lakini Sila na Timoteo wakabaki Beroya. Nao wale waliomwongoza Paulo wakamufikisha mpaka katika muji wa Atene. Kisha wakarudi Beroya wakiwa wameagizwa na Paulo kwamba wawaambie Timoteo na Sila wamufuate upesi. Paulo alipokuwa akingojea Sila na Timoteo kule Atene, moyo wake ukavunjika sana kuona namna muji ule ulivyojaa sanamu za miungu. Alikuwa akibishana na Wayuda katika nyumba ya kuabudia pamoja na watu wa mataifa mengine walioogopa Mungu. Vilevile alibishana kila siku na watu aliowakuta kwenye nafasi ya makutano. Walimu wamoja wa kikundi cha Waepikurio na cha Wastoiko, wakaanza kubishana na Paulo. Wamoja wao wakauliza: “Huyu katetea anataka kusema nini?” Wengine wakasema: “Anaonekana kuwa muhubiri wa miungu ya kigeni.” Walisema hivi kwa sababu Paulo alikuwa akihubiri juu ya Yesu na jinsi alivyofufuka. Halafu wakamukamata Paulo, na kumupeleka mbele ya Baraza Kubwa inayoitwa “Areopago,” wakamwuliza: “Unaweza kutujulisha maana ya mafundisho haya mapya unayotoa? Kwa maana unatuelezea mambo ya kigeni. Basi tunataka kujua maana yake.” (Haya yote ni kwa kuwa wazaliwa wa Atene pamoja na wageni walioishi kati yao, wanapitisha wakati wao wote kwa kueleza na kusikiliza habari mupya mupya.) Halafu Paulo akasimama mbele ya Areopago na kusema: “Ninyi wakaaji wa Atene, ninaona kwamba ninyi ni watu munaopenda sana mambo yote ya dini. Kwa maana nilipokuwa nikipitapita katika muji wenu nilichunguza nafasi zenu za kuabudia, nikaona hata mazabahu mamoja ambako waliyochora maandiko haya: ‘Kwa ajili ya mungu asiyejulikana.’ Basi yule munayemwabudu pasipo kumujua ndiye mimi ninayemuhubiri kwenu sasa. Mungu aliyeumba ulimwengu na vitu vyote vinavyokuwa ndani yake, yeye anayekuwa Bwana wa mbingu na dunia, hakai ndani ya hekalu zilizojengwa na watu. Yeye hahitaji kushugulikiwa na watu, kama vile angekuwa na lazima ya musaada fulani. Kwa maana yeye ndiye anayewapa watu wote pumzi ya uzima, pamoja na vitu vyote wanavyohitaji. Kutokana na mutu mumoja, yeye aliumba watu wa mataifa yote kusudi waishi katika dunia yote. Aliwapangia nyakati na kukata mipaka ya inchi wanayopaswa kukaa ndani yake. Mungu alitaka watafute kumujua, na kama ikiwezekana wamutambue hata ikiwa kama kwa njia ya kupapasa. Na kweli yeye hayuko mbali na kila mumoja wetu, maana ‘kwa uwezo wake tunaishi, tunatenda na kuendelea kuwa.’ Ni sawa na maneno ya watunga mashairi wamoja wa kwenu waliosema: ‘Sisi vilevile tuko watoto wake.’ Basi kwa kuwa sisi tuko watoto wa Mungu, tusiwaze kwamba anafanana na sanamu ya zahabu au ya feza au ya jiwe, iliyochorwa kwa ufundi na akili ya watu. Mungu hahesabu tena nyakati zile watu walipokuwa katika ujinga, lakini sasa anatangaza kwa watu wote, na nafasi zote kwamba wageuke toka zambi zao. Kwa maana amekwisha kupanga siku atakapohukumu dunia kwa haki, kwa njia ya mutu mumoja, yule aliyemuweka kwa kazi ile. Naye amehakikisha mambo hayo kwa kumufufua mutu yule.” Nao waliposikia Paulo akisema juu ya ufufuko, wamoja wakamuchekelea na wengine wakasema: “Tutakusikiliza tena ukisema juu ya habari hii siku ingine.” Ni vile Paulo alivyoachana nao. Ingawa vile watu wamoja walijiunga naye na kuamini. Kati yao kulikuwa Dionisio, mumoja wa Baraza Kubwa inayoitwa Areopago, pamoja na mwanamuke mumoja aliyeitwa Damari na watu wengine vilevile. Nyuma ya mambo hayo, Paulo akatoka Atene, na kwenda katika muji wa Korinto. Kule akakutana na Muyuda aliyeitwa Akila, muzaliwa wa jimbo la Ponto, na jina la muke wake lilikuwa Prisila. Katika siku zile walikuwa wangali wakitoka katika inchi ya Italia, kwa sababu mutawala Klaudio alikuwa ameamuru kwamba Wayuda wote watoke Roma. Paulo akaenda kuwatembelea kwao. Naye akakaa na kutumika pamoja nao, kwa maana wote walikuwa wafundi wa kutengeneza hema. Na kila siku ya Sabato, Paulo alibishana na Wayuda na Wagriki katika nyumba ya kuabudia na kuwashinda. Sila na Timoteo walipofika toka Makedonia, Paulo akajitolea sana kwa kuhubiri Neno la Mungu, akihakikisha kwa Wayuda kwamba Yesu ndiye Kristo. Lakini wakati Wayuda walipingana naye na kumutukana, kwa hiyo akakunguta mavumbi yaliyorukia juu ya nguo zake na kuwaambia: “Lazima ya kuazibiwa kwenu ikuwe juu ya kichwa chenu wenyewe! Mimi sina kosa. Tangu sasa nitawaendea watu wa mataifa mengine.” Halafu Paulo akaondoka pale, akaenda kukaa katika nyumba ya mutu mumoja aliyeitwa Tito Yusto, aliyekuwa mwenye kuogopa Mungu. Nyumba ya mutu huyu ilikuwa karibu sana na nyumba ya kuabudia. Na Krispo, mukubwa wa nyumba ya kuabudia, akamwamini Bwana pamoja na watu wote wa nyumba yake. Nao Wakorinto wengi waliomusikiliza Paulo wakaamini na kubatizwa. Siku moja usiku, Bwana akamwambia Paulo katika maono: “Usiogope, uendelee tu kusema, wala usinyamaze, kwa maana mimi ni pamoja nawe. Hakuna mutu katika muji huu atakayesubutu kukukamata kwa kukutendea vibaya, kwa maana ndani yake kutakuwa watu wengi watakaonigeukia.” Na Paulo akakaa kule kwa muda wa mwaka mumoja na miezi sita, akiwafundisha watu Neno la Mungu. Katika nyakati Galio alipokuwa liwali wa jimbo la Akaya, Wayuda wakamufanyia Paulo shauri baya kwa nia moja, wakamukamata na kumupeleka mbele ya tribinali, na kumushitaki: “Mutu huyu anawavuta watu kumwabudu Mungu kwa njia isiyopatana na Sheria yetu.” Paulo alipotaka kusema, Galio akawaambia Wayuda: “Kama mungemushitaki mutu huyu juu ya neno la uovu au kosa kubwa alilofanya, ningewasikiliza ninyi Wayuda vema. Lakini kwa kuona ni mabishano tu juu ya maneno, majina na sheria yenu, maneno yale yanawaangalia ninyi wenyewe. Mimi sitakata maneno yale.” Na kisha akawafukuza toka ndani ya tribinali. Basi wakamukamata Sositeni, mukubwa wa nyumba ya kuabudia, wakamupiga pale mbele ya tribinali. Lakini Galio hakushugulika na jambo hilo. Paulo akaendelea kule Korinto kwa muda wa siku nyingi. Kisha akaagana na wandugu waamini, akasafiri kwa njia ya chombo na kwenda katika inchi ya Suria. Nao Prisila na Akila walikuwa pamoja naye. Mbele ya kuondoka, Paulo alinyolewa kwenye kivuko cha Kenkurea, kwa maana alikuwa ametimiza kiapo alichofanya mbele ya Mungu. Walipofika Efeso, Paulo akawaacha wale wenzake kule. Naye mwenyewe akaingia ndani ya nyumba ya kuabudia na kubishana na Wayuda. Nao wakamusihi akae nao muda murefu zaidi, lakini hakukubali. Alipoagana nao, akawaambia: “Kama Mungu akitaka nitarudi huku kwenu tena.” Halafu akaondoka Efeso, akisafiri kwa njia ya chombo. Naye alipofika katika muji Kaisaria, akaenda Yerusalema kwa kusalimia kanisa. Kisha akaenda Antiokia. Alipokwisha kukaa Antiokia kwa siku chache, akaondoka kule, akapita muji kwa muji toka katika inchi ya Galatia mpaka katika inchi ya Furigia, na kule akawatia wanafunzi nguvu. Katika siku zile, Muyuda mumoja, jina lake Apolo, muzaliwa wa muji Alesanduria, alikuwa amefika katika muji Efeso. Alikuwa mutu mwenye uwezo katika masemi na mwenye kuelewa sana Maandiko. Mutu huyu alikuwa amefundishwa Njia ya Bwana, naye alitangaza kwa bidii sana na kufundisha kwa ukweli habari za Yesu. Lakini alikuwa akijua tu ubatizo wa Yoane. Yeye akaanza kusema pasipo woga katika nyumba ya kuabudia. Prisila na Akila walipomusikia, wakaenda naye kwao na kumufasiria Njia ya Mungu kwa ukweli zaidi. Apolo alipotaka kwenda katika jimbo la Akaya, wandugu waamini wakamutia moyo, nao wakawaandikia wanafunzi wa kule kwamba wamukaribishe vizuri. Na wakati alipofika kule, akawasaidia sana wale walioamini kwa nguvu ya neema ya Mungu, kwa maana alibishana na Wayuda mbele ya watu wote na kuwashinda kabisa. Aliwaonyesha kwa njia ya Maandiko Matakatifu kwamba Yesu ndiye Kristo. Wakati Apolo alipokuwa Korinto, Paulo akasafiri akipitia katika inchi ya vilima na kufika Efeso. Kule akakuta wanafunzi wamoja; akawauliza: “Ninyi mulipokea Roho Mutakatifu wakati mulipoamini?” Nao wakamujibu: “Hapana! Hatujasikia hata kidogo kwamba kuko Roho Mutakatifu.” Halafu Paulo akawauliza: “Basi mulibatizwa kwa ubatizo gani?” Wakamujibu: “Tulibatizwa kwa ubatizo wa Yoane.” Paulo akawaambia: “Yoane aliwabatiza wale waliogeuka toka zambi zao na kuwaambia Waisraeli kwamba wamwamini yule atakayekuja nyuma yake, naye ndiye Yesu.” Waliposikia maneno haya, walibatizwa kwa jina la Bwana Yesu. Paulo akaweka mikono yake juu yao, na Roho Mutakatifu akashuka juu yao, nao wakaanza kusema kwa luga na kutabiri. Wote walikuwa kadiri ya watu kumi na wawili. Kwa muda wa miezi mitatu Paulo alikuwa akiingia katika nyumba ya kuabudia na kuhubiri watu kwa uhodari. Akabishana nao juu ya habari za Ufalme wa Mungu, akitaka wazisadiki. Lakini wamoja wakakuwa na mioyo migumu hata wakakataa kuamini, wakaanza kusema vibaya juu ya Njia ya Bwana mbele ya mukutano. Kwa hiyo Paulo akajitenga nao, akaenda na wanafunzi peke yao. Na kila siku alibishana na watu katika chumba cha kufanyia usomi cha mutu mumoja aliyeitwa Tirano. Mambo haya yakaendelea kwa muda wa miaka miwili hata Wayuda na Wagriki wote waliokaa katika jimbo la Azia wakasikia neno la Bwana. Mungu akaendelea kufanya miujiza ya ajabu kwa njia ya Paulo. Na hata watu walitwaa vitambaa na nguo zilizogusa mwili wa Paulo, wakazipeleka kwa wagonjwa, nao wakapona na pepo wakatoka ndani yao. Na kulikuwa Wayuda wamoja waliotangatanga huku na huko kwa kufukuza pepo. Watu wale wakajaribu vilevile kutaja jina la Bwana Yesu, wakiwaambia vilevile pepo: “Ninawaamuru muondoke kwa jina la Yesu, yule anayehubiriwa na Paulo.” (Waliofanya hivi walikuwa wana saba wa Sikewa, Kuhani Mukubwa mumoja wa Wayuda.) Lakini yule pepo akawajibu: “Ninamujua Yesu na ninamufahamu Paulo, lakini ninyi ni nani?” Na yule mutu aliyekuwa na pepo ndani yake akawarukia, akawashinda wote nguvu na kuwatendea vibaya hata wakakimbia toka nyumba yake wakiwa uchi na wakijaa vidonda. Wakaaji wote wa Efeso, Wayuda na Wagriki wakajua habari hii. Halafu wote wakashikwa na woga na wakalitukuza jina la Bwana Yesu. Wengi kati ya wale walioamini walikuja kuungama na kutangaza waziwazi mambo waliyofanya. Na watu wengi kati ya wale waliofanya mambo ya uchawi wakaleta vitabu vyao vya uganga na wakavichoma mbele ya watu wote. Bei ya vitabu vile ilipohesabiwa, ikafikia vikoroti vya feza elfu makumi tano. Ni hivi neno la Bwana lilivyoendelea kuenea fasi zote kwa uwezo wake na kuzidi kuonekana kuwa lenye nguvu. Nyuma ya mambo yale, Paulo alikusudia kwenda Yerusalema, akipitia katika inchi ya Makedonia na katika jimbo la Akaya. Akasema: “Nikisha kufika kule, ni lazima niende Roma vilevile.” Halafu akawatuma wawili kati ya wasaidizi wake, Timoteo na Erasto watangulie kwenda Makedonia. Yeye mwenyewe akabaki tena kwa muda katika jimbo la Azia. Katika siku zile kulitokea fujo kubwa kwa ajili ya Njia ya Bwana. Kulikuwa fundi mumoja wa kufua feza, jina lake Demetrio. Alikuwa akitengeneza sanamu ndogo za feza zinazofanana na hekalu la mungu muke Artemi. Na kwa njia ile aliwapatia wafundi faida kubwa. Yeye alikusanya wale wafundi wote pamoja na watu wengine waliofanya kazi sawasawa na ile na kuwaambia: “Wandugu, munajua kwamba sisi tunapata mali mengi kwa njia ya kazi hii. Sasa ninyi wenyewe munaona na kusikia namna huyu Paulo anayofanya. Amekwisha kuwavuta na kuwaonya watu wengi, si hapa Efeso tu, lakini ni karibu katika jimbo lote la Azia. Anasema kwamba miungu inayotengenezwa na watu si miungu hata kidogo. Hivi kunakuwa hatari, na si kwa kazi hii yetu kuzarauliwa tu, lakini vilevile hekalu la mungu mukubwa muke, Artemi, litahesabiwa kuwa kitu bure. Na tena utukufu wake utapunguka, yeye anayeabudiwa na watu wote wa Azia na dunia nzima!” Watu wale waliposikia maneno haya, wakajaa na hasira na kuanza kulalamika wakisema: “Artemi wa Waefeso atukuzwe!” Fujo ikajaa katika muji wote. Wale watu wakawakamata wanainchi wa Makedonia, Gayo na Aristarko waliokuwa wakisafiri pamoja na Paulo. Nao wote pamoja wakawapeleka kwa haraka katika nyumba ya makutano. Paulo alitaka kujionyesha mbele ya lile kundi la watu, lakini wanafunzi wakamukataza. Hata wakubwa wamoja wa jimbo la Azia, waliokuwa warafiki zake wakamutumia ujumbe wakimusihi kwamba asiingie ndani ya nyumba ile. Wakati ule, mukutano ulikuwa umejaa fujo kwa sababu watu wamoja walikuwa wakilalamika na kusema hivi na wengine hivi, na wengi kati yao hawakujua hata ni kwa sababu gani walikusanyika. Watu wamoja katika mukutano wakaeleza mambo yaliyotokea kwa Alesanduro, yeye aliyesukumwa na Wayuda kwenda kusema mbele ya watu. Basi Alesanduro akainua mukono kwa kuwanyamazisha watu, kwa maana alitaka kujitetea mbele yao. Lakini walipotambua kwamba yeye ni Muyuda, wakalalamika wote pamoja kwa muda wa saa mbili, wakisema: “Artemi wa Waefeso atukuzwe!” Kwa mwisho katibu mukubwa wa muji akawatuliza watu, akisema: “Ninyi wanainchi wenzangu wa Efeso, watu wote wanajua kwamba ni wakaaji wa Efeso ndio wanaoshugulika na kulinda hekalu la mungu Artemi na sanamu yake iliyoshuka toka mbinguni. Basi kwa maana hakuna anayeweza kukana maneno haya, ni lazima mutulie, wala musifanye kitu chochote kwa haraka. Kwa maana mumewaleta watu hawa hapa, ingawa hawakuiba vitu vya hekalu, wala kumutukana mungu wetu. Basi ikiwa Demetrio na wafundi wenzake wanakuwa na mashitaki juu ya mutu fulani, tuko na tribinali na wakubwa wako pale. Wanaweza kupeleka mashitaki yao kule! Na kama mukiwa na neno lingine, litakatwa katika mukutano ulioruhusiwa. Kwa maana kufuatana na mambo yaliyotukia leo, tunaweza kushitakiwa kwamba tumeleta fujo. Tena hakuna neno tunaloweza kusema kwa kueleza sababu ya kufanya mukutano huu.” Kisha kusema maneno haya, akaaga mukutano. Fujo ilipokwisha, Paulo akawakusanya wanafunzi na kuwatia moyo. Kisha akaagana nao, akasafiri kwenda Makedonia. Alipita katika inchi ile akiwaambia wanafunzi maneno mengi ya kuwatia moyo. Kisha akaenda Ugriki, na kukaa kule kwa muda wa miezi mitatu. Alipokuwa tayari kuvuka na chombo kwenda katika inchi ya Suria, akapata habari kwamba Wayuda walimufanyia shauri baya. Kwa hiyo akakusudia kurudia, akipitia Makedonia. Na hawa ndio watu waliokwenda pamoja naye: Sopateri mwana wa Piro, wa muji Beroya; Aristarko na Sekundo, wa muji Tesalonika; Gayo, wa muji Derbe; nao Timoteo, Tikiko na Trofimo, wa jimbo la Azia. Watu hawa wakatutangulia kwenda Troa, nao wakatungojea kule. Lakini nyuma ya sikukuu ya Mukate Usiotiwa Chachu, sisi tukaondoka katika muji Filipi kwa njia ya chombo. Na kisha safari ya siku tano tukawakuta Troa, nasi tukakaa kule kwa muda wa siku saba. Siku ya kwanza ya juma, tulikuwa tunakusanyika kwa kumega mukate. Paulo akasemezana na watu na kuendelea kuwahubiria mpaka katikati ya usiku, kwa sababu alikusudia kuondoka kesho yake. Na kulikuwa taa nyingi katika chumba cha gorofi tulichokusanyika ndani yake. Kijana mumoja, aliyeitwa Eutiko, alikuwa akiikaa kwenye dirisha. Na kwa muda ule murefu Paulo alipofundisha, Eutiko akaanza kusinziasinzia na kwa mwisho akawezwa na usingizi na akaanguka chini toka kwenye gorofi ya tatu. Walipomunyanyua alikuwa amekwisha kufa. Paulo akashuka chini, akajilaza juu yake na kumukumbatia akasema: “Musilie kwa maana angali muzima!” Kisha Paulo akapanda juu tena kwenye gorofi, akamega mukate na kuukula. Akaendelea kuhubiri kwa muda murefu mpaka saa za mapambazuko, na kisha akaondoka. Watu wakarudi na yule kijana, akiwa muzima nao wakafarijiwa sana. Sisi tulitangulia tukaingia ndani ya chombo na kusafiri kwenda Asosi. Kule tulipaswa kumutwaa Paulo sawa alivyotuagiza, kwa maana alikuwa amekusudia kwenda kule kwa miguu. Alipokuwa Asosi, tukamwingiza ndani ya chombo na kwenda pamoja naye mpaka Mitilene. Kesho yake tukaondoka kule kwa njia ya chombo na kufika kwenye kisanga cha Kio, na kesho kutwa tukafika kwenye kisanga cha Samosi. Na siku iliyofuata tukafika Mileto. Paulo alikuwa amekusudia kupita Efeso kwa chombo pasipo kuezeka kule, kusudi asikawie katika jimbo la Azia. Kwa maana alikuwa na haraka ya kufika Yerusalema mbele ya siku ya Pentekoste kama ikiwezekana. Toka Mileto, akatuma ujumbe Efeso kwa kuwaita wazee wa kanisa. Nao walipofika, akawaambia: “Ninyi munajua namna nilivyoishi wakati wote nilipokuwa pamoja nanyi, tangia siku ile ya kwanza nilipofika katika jimbo la Azia. Nilimutumikia Bwana kwa unyenyekevu wote na kwa machozi na katika majaribu niliyopata kwa ajili ya mashauri mabaya Wayuda waliyonifanyia. Munajua kwamba sikuwaficha hata neno moja lenye kuwafalia ninyi, lakini niliwahubiri na kuwafundisha katika mikutano na katika nyumba zenu. Nimewaonya Wayuda wa mataifa mengine kwamba wanapaswa kumugeukia Mungu na kumwamini Bwana wetu Yesu Kristo. Basi sasa kwa kuwa ninalazimishwa na Roho Mutakatifu, nitakwenda Yerusalema pasipo kujua mambo yatakayonitokea kule. Lakini kitu kimoja ninachojua tu, ni kwamba katika kila muji Roho Mutakatifu ananihakikishia kwamba vifungo na mateso vinaningojea. Lakini sihesabu maisha yangu kuwa kitu cha bei kali kwangu. Shabaha moja ninayokuwa nayo ni kufikia mwisho wa utumishi wangu na kutimiza kazi ile niliyopewa na Bwana Yesu; maana yake kushuhudia Habari Njema ya neema ya Mungu. “Nilikuwa nikizungukazunguka kati yenu ninyi wote nikitangaza Ufalme wa Mungu. Lakini sasa, ninajua kwamba hakuna hata mumoja atakayeniona tena. Ndiyo maana ninahakikisha mbele yenu leo kwamba mimi sitabeba lazima ya damu ya hata mumoja wenu atakayepotea. Ni vile kwa sababu niliwatangazia mupango wote wa Mungu pasipo kuwaficha kitu. Mujichunge ninyi wenyewe na muchunge vilevile lile kundi lote Roho Mutakatifu alilowapatia kusudi mukuwe wasimamizi wao. Hivi mutaweza kuchunga kanisa la Mungu ambalo alijipatia kwa damu ya Mwana wake. Ninajua kwamba nyuma ya kuondoka kwangu, imbwa wakali wa pori wataingia katikati yenu, nao hawatahurumia kundi lile. Na hata kati yenu kutatokea watu watakaotoa mafundisho ya kupotosha wengine kusudi wawavute waamini kuwafuata. Kwa sababu hii mujiangalie, mukikumbuka kwamba kwa muda wa miaka mitatu, usiku na muchana, sikuchoka kumwonya kila mumoja wenu kwa machozi. “Basi sasa ninawaweka chini ya ulinzi wa Mungu na wa neno lake la neema linaloweza kuwajenga katika imani na kuwapa urizi pamoja na watu wake wote watakatifu. Mimi sikutamani feza, zahabu, wala nguo ya mutu yeyote. Ninyi wenyewe munajua namna nilivyotumika kwa mikono yangu mimi peke kwa kupata vitu vyote ambavyo mimi pamoja na wenzangu tulihitaji. Katika mambo hayo yote niliyofanya, nimewaonyesha mufano kwamba tunapaswa kusumbuka vile na kazi kwa kuwasaidia wasiojiweza, tukikumbuka maneno haya Bwana Yesu mwenyewe aliyosema: ‘Ni heri kutoa kuliko kupewa.’ ” Paulo alipokwisha kusema maneno haya, akapiga magoti pamoja nao wote na kuomba. Na wote walilia sana wakimukumbatia na kumubusu. Walihuzunika zaidi kwa sababu aliwaambia kwamba hawatamwona tena. Wakamusindikiza mpaka kwenye chombo. Tulipokwisha kuagana nao, tukasafiri ndani ya chombo na kwenda mara moja mpaka kwenye kisanga cha Kosi. Kesho yake tukafika katika muji Rodo, na kutoka kule tukafika katika muji Patara. Kule tukakuta chombo kilichokuwa kikienda katika inchi ya Foinikia; tukaingia ndani yake na kusafiri. Tulipoanza kuona kisanga cha Kipuro, tukikiacha kwa upande wa kusini na kuelekea katika jimbo la Suria. Tukaezeka kwenye kivuko cha Tiro, kwa maana ni pale chombo kilipaswa kupakuliwa mizigo. Kule tukakuta wanafunzi na tukakaa pamoja nao muda wa juma moja. Nao wakiogozwa na Roho Mutakatifu wakamwambia Paulo asiende Yerusalema. Lakini muda ule ulipotimia tukaondoka na kuendelea na safari yetu. Waamini wote pamoja na wanawake na watoto wao wakatusindikiza mpaka mbali na hata kufika kwenye kivuko cha muji. Kule sisi wote tukapiga magoti na kuomba. Kisha kuagana, tukaingia ndani ya chombo, nao wakarudi kwao. Kutoka Tiro tukaendelea hata tukafika Tolemai. Na pale tukamaliza safari yetu ya bahari. Kule tulisalimia wandugu zetu waamini na kukaa nao muda wa siku moja. Kesho yake tukaondoka na kufika katika muji Kaisaria. Kule tukaenda kupanga katika nyumba ya muhubiri Filipo, aliyekuwa mumoja kati ya wale watu saba waliochaguliwa Yerusalema. Yeye alikuwa na wabinti wane waliokuwa hawajaolewa waliokuwa na zawadi ya kutabiri. Nasi tulipokuwa tumekwisha kukaa kule siku nyingi, nabii mumoja, aliyeitwa Agabo, akafika kutoka Yudea. Akatufikia, akatwaa mukaba wa Paulo, akajifunga miguu na mikono yake mwenyewe na kusema: “Roho Mutakatifu anasema: ‘Wayuda watamufunga mutu mwenye mukaba huu namna hii kule Yerusalema na kumutoa kwa watu wa mataifa mengine.’ ” Basi tuliposikia maneno hayo, sisi pamoja na watu wa Kaisaria tukamusihi Paulo asiende Yerusalema. Lakini Paulo akajibu: “Kwa sababu gani munalia na kunivunja moyo? Mimi niko tayari, si kwa kufungwa tu kule Yerusalema, lakini hata kufa vilevile kwa ajili ya jina la Bwana Yesu.” Tulipoona kwamba amekataa shauri letu, tukanyamaza na kusema: “Mapenzi ya Bwana yafanyike.” Nyuma ya siku zile tulizokaa kule tukafunga mizigo yetu na kwenda Yerusalema. Wanafunzi wamoja toka muji Kaisaria wakatusindikiza na kutufikisha kwa Munasoni, mutu wa Kipuro, aliyegeuka mwamini tangu siku nyingi, kusudi tupate kupanga kwake. Tulipofika Yerusalema, wandugu waamini wakatupokea kwa furaha. Kesho yake tukaenda pamoja na Paulo kwa Yakobo, na wazee wote wa kanisa walikuwa kule vilevile. Kisha kuwasalimu, Paulo akaanza kuwaelezea neno kwa neno mambo yote, Mungu aliyofanya kati ya mataifa mengine kwa njia ya kazi yake. Nao waliposikia maneno hayo, wakamusifu Mungu. Na kisha wakamwambia Paulo: “Ndugu, unaona namna maelfu ya Wayuda walivyoamini; nao wote wanajitolea sana kwa kushika Sheria. Lakini wamesikia habari juu yako kwamba unawafundisha Wayuda wote wanaokaa katika inchi za mataifa wasishike Sheria ya Musa. Umewakataza wasiwatahiri watoto wao wala kufuata desturi zetu za kiyuda. Hakika watu wale watasikia kwamba umekwisha kufika. Basi tufanye nini? Kwa hiyo, ufanye kama hivi tunavyotaka kukuambia. Hapa tuko na watu wane waliofanya kiapo mbele ya Mungu. Kwenda ujiunge na watu wale katika ibada ya utakaso, nawe uwalipie malipo yanayoamuriwa kusudi wapate kunyolewa. Hivi watu wote watajua kwamba habari zile walizoambiwa juu yako zilikuwa za uongo mutupu. Na zaidi ya hii watajua kwamba unafuata Sheria ya Musa katika maisha yako. Lakini kwa ngambo ya watu wa mataifa mengine walioamini, tumekwisha kuwaandikia juu ya mambo tuliyoamua. Tumewaamuru kwamba wasikule vyakula vilivyotolewa kwa kutambikia sanamu; wasikule damu wala nyamafu; na waepuke uasherati.” Halafu kesho yake Paulo akaenda na wale watu wane, na akajitakasa pamoja nao. Kisha akaingia ndani ya hekalu na kutangaza wakati siku za utakaso zitakapotimia, na sadaka itakayotolewa kama malipo kwa ajili ya kila mumoja wao. Zile siku saba zilipokaribia kutimia, Wayuda wamoja waliotoka katika jimbo la Azia wakamwona Paulo ndani ya hekalu. Wao wakashawishi watu wote waliokusanyika, wakamukamata wakilalamika: “Ninyi wanainchi Waisraeli, mutusaidie! Huyu ndiye mutu yule anayefundisha kwa watu wote, nafasi zote maneno ya kuzarau taifa letu, Sheria ya Musa, na hekalu hili. Na zaidi ya hii, amewaingiza watu wa mataifa mengine katika hekalu na hivi amechafua Pahali hapa Patakatifu!” (Walisema hivi kwa sababu walikuwa wamemwona Paulo katika muji pamoja na Mwefeso mumoja aliyeitwa Trofimo, nao walizani kwamba Paulo alikuwa amemwingiza katika hekalu.) Muji wote ukajaa fujo na watu wakakusanyika pale mbiombio. Wakamukamata Paulo na kumukokotea mpaka inje ya hekalu, na mara moja wakafunga milango yake. Walipotafuta kumwua Paulo, habari ikamufikia mwongozi wa kundi la waaskari kwamba muji wote wa Yerusalema umejaa fujo. Mara moja akatwaa waaskari pamoja na wakubwa wao na kwenda nao haraka pale watu walipokusanyika. Nao walipomwona huyo mwongozi pamoja na waaskari wake wakaacha kumupiga Paulo. Halafu huyo mwongozi akamujongelea Paulo, akamukamata na kuamuru afungwe na minyororo miwili. Kisha akauliza: “Mutu huyu ni nani? Naye amefanya nini?” Wamoja katika makutano walikuwa wakilalamika na kusema hivi, na wengine hivi. Basi kwa kuwa yule kiongozi hakuweza kupata jibu kamili kwa sababu ya makelele, akaamuru kwamba wamupeleke Paulo ndani ya upango wa waaskari. Paulo alipofika kwenye ngazi, waaskari walilazimishwa kumubeba kwa sababu makutano yalitomboka sana. Maana wote walimufuata nyuma wakilalamika: “Auawe!” Waaskari walipotaka kumwingiza Paulo katika upango, akamwuliza mukubwa wa kundi la waaskari: “Unaweza kuniruhusu kukuambia neno moja?” Yule mukubwa wa kundi la waaskari akamwuliza: “Unajua Kigriki? Wewe si yule Mumisri aliyeleta fujo siku hizi na kuwaongoza wauaji elfu ine kwenda naye katika jangwa?” Paulo akajibu: “Mimi ni Muyuda, muzaliwa wa muji Tarso, katika jimbo la Kilikia. Ninatoka katika muji unaosifiwa sana. Tafazali uniruhusu kusema na watu hawa.” Yule mukubwa wa kundi la waaskari akamuruhusu. Basi Paulo akasimama juu ya ngazi, akainua mukono kwa kuwaalika watu wanyamaze. Na watu waliponyamaza kabisa, Paulo akawaambia maneno haya katika luga ya Kiebrania: “Wandugu zangu na wababa zangu, musikilize yale ninayotaka kusema kwa kujitetea mbele yenu.” Walipomusikia akisema nao katika luga ya Kiebrania, wakanyamaza zaidi. Halafu Paulo akasema: “Mimi ni Muyuda, nimezaliwa Tarso, katika jimbo la Kilikia, lakini nililelewa katika muji huu wa Yerusalema. Mimi nilikuwa mwanafunzi wa Gamalieli, na alinifundisha namna ya kufuata kabisa Sheria ya babu zetu. Nikajitolea kabisa kwa kutumikia Mungu kama vile ninyi wote munavyofanya leo. Mimi niliwatesa hata kuwaua watu waliofuata Njia ya Bwana. Niliwakamata wanaume na wanawake na kuwatupa katika kifungo. Hata Kuhani Mukubwa pamoja na baraza lote la wasimamizi wa watu wanaweza kushuhudia kwamba ninasema kweli. Nilipata hata barua toka kwao iliyoandikwa kwa ajili ya wandugu Wayuda wa Damasiki. Nikaenda kule kusudi niwafunge waamini waliokuwa kule na kuwaleta mpaka Yerusalema wapate kuazibiwa. “Nilipokuwa katika safari karibu kufika Damasiki, yapata saa sita ya muchana, kwa rafla mwangaza mukubwa toka mbinguni ukanizunguka. Nikaanguka chini, nikasikia sauti ikiniambia: ‘Saulo, Saulo, kwa sababu gani unanitesa?’ Nami nikauliza: ‘Wewe ni nani, Bwana?’ Na Bwana akanijibu: ‘Mimi ni Yesu wa Nazareti unayemutesa.’ Watu waliokuwa pamoja nami wakaona mwangaza ule, lakini hawakusikia sauti ya yule aliyekuwa akinisemesha. Nikauliza: ‘Bwana, nifanye nini?’ Naye Bwana akanijibu: ‘Simama, uende Damasiki, na kule watakuambia mambo yote Mungu anayokuagiza kufanya.’ Na kwa kuwa nilikuwa sioni tena kwa sababu ya ukali wa ule mwangaza, wenzangu wakanishika mukono na kuniongoza mpaka nikafika Damasiki. “Kule Damasiki kulikuwa mutu mumoja aliyeitwa Anania, mutu aliyeogopa Mungu na mwenye kushika Sheria yetu. Aliheshimiwa sana na Wayuda wote waliokaa kule. Yeye akanifikia, akasimama karibu nami na kuniambia: ‘Ndugu yangu Saulo, upate kuona tena!’ Na saa ile ile nikapata kuona na kuweza kumwona. Kisha akasema: ‘Mungu wa babu zetu amekwisha kukuchagua wewe kusudi ujue mapenzi yake. Anataka umwone Mwenye Haki, na kumusikia akisema kwa kinywa chake mwenyewe. Kwa maana utatoa ushuhuda wake kwa watu wote, utasema juu ya mambo yale uliyoona na kuyasikia. Basi sasa, unangojea nini? Simama ubatizwe na kuondolewa zambi zako, ukiomba kwa jina la Bwana.’ ” “Nilipokuwa nimekwisha kurudia Yerusalema, na nilipokuwa nikiomba katika hekalu, nikapata maono. Nikamwona Bwana, naye akaniambia: ‘Fanya haraka uondoke upesi katika muji huu Yerusalema kwa sababu watu wake hawatakubali ushuhuda utakaoutoa juu yangu.’ Nami nikajibu: ‘Bwana, watu hawa wanajua wazi kwamba nilikuwa nikipitapita katika nyumba za kuabudia kwa kuwafunga na kuwapiga wale wanaokuamini. Na wakati watu walipomwua Stefano, aliyetoa ushuhuda juu yako, mimi mwenyewe nilikuwa pale, nami nilikuwa nimekubaliana nao juu ya kuuawa kwake. Na zaidi ya ile ni mimi niliyechunga nguo za wale waliomwua.’ Halafu Bwana akaniambia: ‘Kwenda, kwa maana nitakutuma mbali kwa watu wa mataifa mengine.’ ” Makutano walimusikiliza Paulo mpaka aliposema maneno yale. Kisha wakasema kwa nguvu: “Mumuteketeze mutu huyu! Mumwue, kwa maana hastahili kuishi!” Wakalalamika sana, wakatupatupa nguo zao na kurusha mavumbi juu. Yule mukubwa wa jeshi akaamuru waaskari wamupeleke Paulo katika upango wao. Akaamuru vilevile wamupige fimbo, kusudi apate kujua sababu gani watu walilalamika vile kwa ajili yake. Lakini walipokwisha kumufunga Paulo na kamba kusudi wamupige, yeye akamwambia jemadari mumoja aliyekuwa pale: “Sheria inawaruhusu kumupiga mwanainchi wa Roma, ingawa hajahukumiwa bado?” Yule jemadari aliposikia maneno hayo akaenda kwa yule mukubwa wa jeshi kwa kumupasha na kumwuliza: “Unataka kufanya nini? Mutu huyu ni mwanainchi wa Roma!” Basi jemadari akamwendea Paulo kumwuliza: “Uniambie ukweli, wewe ni mwanainchi wa Roma?” Paulo akamujibu: “Ndiyo.” Halafu mukubwa wa jeshi akasema: “Mimi nilinunua haki ya kuwa mwanainchi wa Roma kwa feza nyingi.” Paulo akamwambia: “Mimi ni mwanainchi wa Roma kwa kuzaliwa.” Mara moja wale waliotaka kumusambisha kwa kumupiga fimbo wakamwacha. Yule mukubwa wa jeshi akaogopa alipotambua kwamba Paulo ni mwanainchi wa Roma, na kwamba alikuwa anamufunga na minyororo. Kesho yake, jemadari alitaka kujua mashitaki kamili ya Wayuda juu ya Paulo. Kwa hiyo akamufungua na kuamuru wakubwa wa makuhani pamoja na Baraza Kubwa wafanye mukutano. Kisha akamuleta Paulo na kumusimamisha mbele yao. Paulo akawakazia macho wale washauri wa Baraza Kubwa na kusema: “Wandugu zangu, mpaka leo zamiri yangu hainihukumu juu ya kitu chochote kinachoelekea mwenendo wangu mbele ya Mungu.” Paulo aliposema maneno hayo, Kuhani Mukubwa Anania akawaamuru wale waliosimama karibu naye wamupige kofi kwenye kinywa. Halafu Paulo akamwambia: “Mungu yeye mwenyewe atakupiga kofi, wewe unayeonekana kwa inje kama ukuta uliopakaliwa chokaa! Wewe unaikaa pale kwa kunihukumu kufuatana na Sheria. Lakini wewe mwenyewe unaivunja kwa kuamuru wanipige!” Watu waliokuwa wakisimama karibu na Paulo wakamwambia: “Wewe unamutukana Kuhani Mukubwa wa Mungu!” Paulo akasema: “Wandugu zangu, sikujua kwamba yeye ni Kuhani Mukubwa. Kwa maana imeandikwa katika Maandiko Matakatifu: ‘Usimulaani mukubwa wa taifa lako.’ ” Halafu Paulo alikuwa akijua kwamba watu wamoja katika Baraza Kubwa walikuwa Wasadukayo na wengine Wafarisayo. Kwa hiyo akasema kwa sauti katika baraza: “Wandugu zangu, mimi ni Mufarisayo, mwana wa Mufarisayo. Mimi ninahukumiwa kwa sababu ninatumaini kwamba wafu watafufuka.” Alipokwisha kusema maneno hayo, kukatokea ugomvi kati ya Wafarisayo na Wasadukayo, nao mukutano ukagawanyika. (Ilitokea vile kwa maana Wasadukayo wanasema kwamba wafu hawatafufuka na kwamba hakuna wamalaika, wala roho; lakini Wafarisayo wanakubali mambo hayo yote.) Basi kukakuwa makelele mengi, na walimu wamoja wa Sheria waliokuwa wa chama cha Wafarisayo wakasimama na kubishana kwa nguvu, wakisema: “Hatuoni ubaya wowote juu ya mutu huyu. Labda roho au malaika wamesema naye!” Ugomvi ulipozidi sana, jemadari akaogopa kwamba watu wale watamurarua Paulo. Kwa hiyo akaamuru waaskari waende katikati ya mukutano ule na kumwondosha Paulo kwa kinguvu katikati yao na kumurudisha ndani ya upango wa waaskari. Usiku ule ule Bwana akamutokea Paulo, akamwambia: “Ujipe moyo! Sawa vile ulivyotoa ushuhuda juu yangu hapa Yerusalema, ni vile vile utakavyopaswa kuutoa katika Roma.” Kesho yake kulipokucha, Wayuda wakafanya shauri; wakafanya kiapo kwamba hawatakula wala kunywa mpaka wamwue Paulo kwanza. Na wale waliofanya shauri lile walikuwa zaidi ya watu makumi ine. Wakaenda kuwaona Makuhani Wakubwa na wasimamizi wa watu na kuwaambia: “Sisi tumefanya kiapo; hatutasubutu kula kitu chochote mpaka tumwue Paulo kwanza. Basi sasa, ninyi pamoja na Baraza Kubwa mumwombe jemadari awaletee Paulo, mukimwambia tu kwamba munataka kuchunguza vizuri zaidi maneno yake. Na sisi tuko tayari kumwua mbele hajafika hapa.” Lakini mupwa wa Paulo akapata habari ya vile watu wale wanavyovizia kumwua Paulo. Halafu akaenda katika upango wa waaskari na kumujulisha Paulo habari ile. Basi Paulo akaita mumoja wa wakubwa wa waaskari na kumwambia: “Umupeleke kijana huyu kwa jemadari kwa maana yuko na neno la kumwambia.” Yule mukubwa akaenda pamoja naye kwa jemadari na kumwambia: “Yule mufungwa Paulo aliniita, akaniomba nikuletee kijana huyu kwa sababu yuko na neno la kukuambia.” Jemadari akamushika yule kijana mukono akaenda naye pembeni na kumwuliza: “Uko na habari gani ya kuniambia?” Kijana akasema: “Wayuda wamepatana kukuomba umulete Paulo kesho katika Baraza Kubwa. Nao watakuambia tu kwamba wakubwa wa baraza wanataka kuchunguza vizuri zaidi maneno yake. Lakini wewe usikubali ombi lao, kwa sababu kuna watu zaidi ya makumi ine wanaovizia kumwua. Watu hawa wamefanya kiapo kwamba hawatakula wala kunywa mpaka wamwue Paulo kwanza.” Yule jemadari akamwagiza yule kijana kwamba asimwambie mutu yeyote kwamba amemupasha habari hiyo, kisha akaagana naye. Kisha jemadari akawaita wakubwa wawili wa waaskari wake, akawaambia: “Mutayarishe waaskari mia mbili, waaskari wapanda-farasi makumi saba, na waaskari wapiga mikuki mia mbili kwa kwenda Kaisaria saa tatu ya usiku. Mutayarishe vilevile farasi wa kumubeba Paulo kusudi afike salama kwa liwali Feliki.” Naye akaandika barua hii: “Mimi Klaudio Lusia, ninakuandikia wewe muheshimiwa Liwali Feliki, pokea salamu zangu. Wayuda walikuwa wamemukamata mutu huyu na kutaka kumwua. Nami nilipopata habari kwamba yeye ni mwanainchi wa Roma, nikaenda na kundi la waaskari na kumwokoa. Na kwa kuwa nilitaka kujua sababu gani Wayuda walimushitaki, nikamufikisha mbele ya Baraza yao Kubwa. Nikatambua kwamba wamemushitaki juu ya ubishi wenye kuelekea Sheria yao, lakini hakutenda kosa lolote linalomupasa kuuawa wala kufungwa. Na wakati nilipopata habari kwamba Wayuda wanafanya shauri la kumwua, mara moja nikakusudia kumutuma kwako, nami nimewaagiza watu wanaomushitaki walete mashitaki yao kwako.” Basi wale waaskari wakafanya kama vile walivyoamuriwa. Wakamutwaa Paulo, na usiku ule ule wakamufikisha mpaka Antipatiri. Kesho yake waaskari waliotembea kwa miguu wakarudi Yerusalema kwenye upango wa waaskari. Wakawaacha waaskari wapanda-farasi waendelee pamoja na Paulo. Nao walipofika Kaisaria, wakamupa liwali ile barua na kumuleta Paulo kwake. Liwali akasoma barua ile na kumwuliza Paulo: “Wewe ni mutu wa jimbo gani?” Aliposikia kwamba yeye ni mutu wa jimbo la Kilikia, akamwambia: “Nitakusambisha wakati wale wanaokushitaki watakapofika.” Kisha akaamuru Paulo alindwe katika nyumba ya kifalme ya Herode. Kulipopita siku tano, Kuhani Mukubwa Anania akaenda Kaisaria pamoja na wasimamizi wamoja wa watu na mutetezi mumoja wa sheria aliyeitwa Tertulo. Nao wakafika mbele ya liwali Feliki kwa kumushitaki Paulo. Walipomwita Paulo, Tertulo akaanza kumushitaki, akisema: “Muheshimiwa Feliki, kwa njia yako tumepata amani ya kweli. Na kwa uongozi wako umeleta mabadiliko mengi mazuri kwa ajili ya taifa hili. Kwa yote hatutasahau mambo hayo yote kila wakati na kila fasi, nasi tunakushukuru sana. Lakini, sababu sitaki kukupotezea wakati murefu, ninakusihi usikilize kwa wema wako maneno tutakayosema kwa kifupi. Tumetambua kwamba mutu huyu ni wa hatari sana, ameanzisha fujo kati ya Wayuda wote katika dunia. Tena yeye ni mukubwa wa chama cha Wanazareti. Naye alijaribu kuchafua hekalu, lakini tukamukamata. [Tulitaka kumuhukumu kufuatana na Sheria yetu, lakini jemadari Lusia alijitokeza na kumwondoa kati yetu kwa kinguvu. Kisha akaamuru kwamba wale wanaomushitaki wakuje kwako.] Na wewe mwenyewe utaweza kumusambisha mutu huyu, na kufahamu vizuri mambo yale tunayomushitakia.” Wayuda wakamwunga mukono, wakisema kwamba maneno yale yote ni ya kweli. Kisha liwali akamufanyia Paulo alama kwa kumuruhusu kusema, naye akasema: “Ninajua kwamba wewe umekuwa mwamuzi wa taifa hili tangia miaka mingi. Sababu hii sina wasiwasi kwa kujitetea mbele yako. Kama unavyoweza kuhakikisha wewe mwenyewe, hakujapita zaidi ya siku kumi na mbili tangu nilipoenda Yerusalema kwa kumwabudu Mungu. Watu hawa hawakunikuta ndani ya hekalu wala ndani ya nyumba za kuabudia, wala nafasi ingine katika muji nikibishana na mutu au nikisukuma watu kufanya fujo. Nao hawawezi kuhakikisha maneno wanayonishitakia sasa. Lakini ninakubali mbele yako kwamba ninamutumikia Mungu wa babu zetu nikifuata Njia ile wanayosema kwamba ni ya uongo. Mimi ninaamini maneno yote yaliyoandikwa katika kitabu cha Sheria na katika vitabu vya manabii. Ninatumaini toka kwa Mungu sawa vile watu hawa wanavyotumaini, kwamba watu wema na wabaya wote watafufuliwa. Kwa sababu hii ninajikaza siku zote kuishi maisha safi bila kuhukumiwa na zamiri yangu mbele ya Mungu na mbele ya watu. “Nyuma ya kupitisha miaka mingi mbali na muji, nilirudi kule Yerusalema kuwaletea watu wa taifa langu musaada wa mali na kumutolea Mungu sadaka. Na wakati ule nilipokuwa nikifanya mambo hayo, walinikuta katika hekalu, nami nilikuwa nimekwisha kufanya ibada ya kutakaswa. Sikukuwa na kundi la watu wala kuleta fujo. Lakini Wayuda wamoja waliotoka katika jimbo la Azia walikuwa pale, na ni hao ndio wangepaswa kuja mbele yako kunishitaki ikiwa wako na neno lolote juu yangu. Au watu hawa wanaokuwa hapa waseme kosa waliloniona nalo wakati niliposambishwa mbele ya Baraza Kubwa. Neno moja tu nililosema kwa sauti nilipokuwa nikisimama ni hili: ‘Ninahukumiwa leo kwa sababu ninatumaini kama wafu watafufuliwa.’ ” Halafu Feliki, aliyekuwa akifahamu vizuri mambo yanayoelekea Njia ya Bwana, akaamuru maneno yale yarudiliwe, akisema: “Nitakata maneno yenu wakati jemadari Lusia atakapokuja.” Kisha akamwamuru yule mukubwa wa jeshi kwamba wamulinde Paulo katika kifungo wakimwachia uhuru kidogo, na wasiwazuize warafiki zake kumusaidia. Nyuma ya siku chache, liwali Feliki akakuja pamoja na muke wake Drusila, aliyekuwa Muyuda. Akaamuru wamwite Paulo, naye akasikiliza maneno aliyosema juu ya kumwamini Kristo Yesu. Lakini Paulo alipokuwa akihubiri juu ya haki, juu ya kujizuiza na juu ya siku ya hukumu ya Mungu itakayokuja, Feliki akaogopa na kumwambia: “Kwa sasa unaweza kujiendea. Nitakuita tena nitakapopata wakati.” Vilevile alikuwa akitazamia kwamba Paulo atamupatia feza. Ni kwa sababu hii alimwita kila mara kwa kuzungumuza naye. Kulipopita miaka miwili, Porkio Festo akamukomboa Feliki kama liwali. Na kwa sababu Feliki alitaka kujipendekeza kwa Wayuda, akamwacha Paulo katika kifungo. Siku tatu nyuma ya kufika kwake katika jimbo lile, Festo akaondoka Kaisaria na kwenda Yerusalema. Kule wakubwa wa makuhani na wakubwa wa Wayuda wakamushitaki Paulo mbele yake. Wakamusihi Festo awafanyie wema kwa kuwaletea Paulo Yerusalema, kwa maana walikuwa wakivizia kumwua katika njia. Festo akajibu: “Paulo analindwa katika kifungo kule Kaisaria, na mimi mwenyewe nitaenda kule sasa hivi. Basi wamoja kati ya wakubwa wenu waende pamoja nami Kaisaria nao wamushitaki kule ikiwa alifanya ubaya wowote.” Kisha kukaa pamoja nao muda wa siku nane au kumi, Festo akarudi Kaisaria. Kesho yake akaikaa ndani ya tribinali na kuamuru wamulete Paulo. Wakati Paulo alipofika, wale Wayuda waliotoka Yerusalema wakamuzunguka na kutoa mashitaki mengi mazito juu yake ambayo wao hawawezi kuhakikisha. Halafu Paulo akajitetea, akisema: “Mimi sikufanya kosa lolote juu ya Sheria ya Musa, juu ya hekalu, wala juu ya Mufalme wa Roma.” Festo aliyetaka kujipendekeza kwa Wayuda, akamwuliza Paulo: “Unataka niende kukusambishia maneno haya kule Yerusalema?” Paulo akajibu: “Mimi ninasimama mbele ya tribinali ya Mufalme wa Roma, na ni hapa ninapopaswa kusambishwa. Sikuwakosea Wayuda kosa lolote, kama vile wewe mwenyewe unavyojua vizuri. Kama mimi ni mukosaji au nimefanya kitendo kinachonipasa kuuawa, mimi sikatai kufa. Lakini kama hakuna ukweli wowote katika mashitaki yao juu yangu, hakuna mutu anayeweza kunitoa kwao. Ninaomba kusambishwa na Mufalme wa Roma.” Basi Festo alipokwisha kukata shauri pamoja na washauri wake, akajibu: “Unaomba kusambishwa na Mufalme wa Roma, basi utakwenda kwa Mufalme wa Roma.” Kulipopita siku chache, mufalme Agripa na dada yake Berenike wakafika Kaisaria kumusalimia Festo. Kufuatana na vile walikaa kule siku nyingi, Festo akamwelezea mufalme maneno ya Paulo. Akamwambia: “Hapa kuna mutu mumoja aliyeachwa na Feliki katika kifungo. Wakati nilipokwenda Yerusalema, wakubwa wa makuhani na wazee wa Wayuda walimushitaki na kuniomba nimuhukumu. Nami nikawajibu kwamba si desturi ya Waroma kumutoa mutu yeyote aliyeshitakiwa mbele ya kusamba uso kwa uso na washitaki wake na kupata nafasi ya kujitetea juu ya jambo walilomushitakia. Basi walipofika hapa pamoja nami, sikupoteza wakati lakini kesho yake nikaikaa ndani ya tribinali na kuamuru wamulete mutu yule. Nao washitaki wake waliposimama, hawakumushitaki juu ya neno baya kama nilivyokuwa ninawazia. Walikuwa tu wakibishana naye juu ya dini yao wenyewe na juu ya mutu mumoja aliyeitwa Yesu; lakini Paulo alidai kwamba yuko muzima. Kwa ngambo yangu sikujua nifanye nini kwa kuchunguza ukweli wa mabishano hayo. Nikamwuliza Paulo kama anataka kwenda Yerusalema kusambishwa kule juu ya maneno yale. Lakini wakati Paulo alipoomba maneno yake yakatwe na Mufalme wa Roma, nikaamuru alindwe katika kifungo mpaka nitakapomutuma kwa Mufalme wa Roma.” Halafu Agripa akamwambia Festo: “Na mimi vilevile ningependa kumusikiliza mutu huyu peke yangu.” Festo akajibu: “Utamusikiliza kesho.” Basi kesho yake Agripa pamoja na Berenike walifika katika shangwe kubwa na kuingia katika chumba cha mukutano, pamoja na wakubwa wa jeshi, na wakubwa wa muji. Festo akaamuru wamulete Paulo. Halafu Festo akasema: “Mufalme Agripa, na ninyi wote munaokuwa hapa pamoja nasi, munamwona mutu huyu Wayuda wote waliyemushitaki kwangu kule Yerusalema na hapa vilevile wakilalamika kwamba hastahili kuishi tena. Mimi niliona kwamba hakufanya kitendo chochote cha kustahili kufa. Lakini kwa sababu yeye mwenyewe aliomba maneno yake yakatwe na Mufalme wa Roma, nilikusudia kumutuma kwake. Mimi sina maneno kamili ya kumwandikia Mufalme wa Roma juu yake. Ndiyo maana nimemuleta mbele yenu na zaidi mbele yako, wewe mufalme Agripa, kusudi kisha kumwuliza, nipate maneno ya kuandika. Kwa sababu ninaona kwamba haina maana kumutuma mufungwa pasipo kueleza wazi mashitaki juu yake.” Agripa akamwambia Paulo: “Sasa unaweza kueleza maneno yako.” Basi Paulo akanyoosha mukono na kuanza kujitetea, akisema: “Mufalme Agripa, ninafurahi sana kusimama mbele yako leo kwa kujitetea juu ya mambo yote Wayuda waliyonishitakia. Ninafurahi zaidi kwa sababu wewe unajua sana desturi zote za Wayuda na mabishano yao yote. Basi ninakuomba unisikilize kwa uvumilivu. “Wayuda wote wanajua maisha yangu tangu mwanzo wa ujana wangu. Wanajua namna nilivyoishi kati ya taifa langu katika Yerusalema. Wamenijua tangu zamani na kama wakitaka wanaweza kushuhudia kwamba nilikuwa mushiriki wa chama cha Wafarisayo, kinachotia mukazo sana juu ya kushika desturi za dini yetu. Na sasa ninasimama hapa kuhukumiwa kwa sababu ninatumainia ile ahadi Mungu aliyotoa kwa babu zetu. Makabila yetu kumi na mawili wanamwabudu Mungu usiku na muchana, kwa maana wanatumaini kuona utimilifu wa ile ahadi. Na ni kwa sababu ya tumaini lile, Ee mufalme, Wayuda wananishitaki. Kwa sababu gani ninyi munazani kwamba haiwezekani kwa mutu kusadiki kwamba Mungu anawafufua wafu? “Kweli mimi mwenyewe niliwaza kwamba nilipaswa kufanya yote ninayoweza kwa kupinga jina la Yesu wa Nazareti. Na ni vile nilivyofanya katika Yerusalema. Nilipata mamlaka toka kwa wakubwa wa makuhani; nami nikawatia watu watakatifu wengi wa Mungu katika kifungo. Na wakati walipowaua mimi nilikubali kwamba wanastahili kuuawa. Mara nyingi niliwaazibu katika nyumba za kuabudia na kuwashurutisha wakane imani yao. Niliwakasirikia kupita kipimo, hata nikaenda kuwatesa katika miji ya inchi za kigeni. “Basi kufuatana na kusudi, nikaenda katika muji Damasiki kwa amri na mamlaka ya wakubwa wa makuhani. Ee mufalme, nilipokuwa katika njia, ilipotimia saa sita ya muchana, nikaona mwangaza unaotoka mbinguni unaopita mwangaza wa jua. Mwangaza ule ukanizunguka pamoja na wenzangu waliosafiri nami. Sisi wote tukaanguka chini, na nikasikia sauti iliyoniambia hivi katika luga ya Kiebrania: ‘Saulo, Saulo, kwa sababu gani unanitesa? Unajiumiza bure kama ngombe anayepiga teke kwenye chongo ya fimbo ya mwenyeji wake.’ Halafu nikauliza: ‘Wewe ni nani, Bwana?’ Na Bwana akajibu: ‘Mimi ni Yesu, unayemutesa. Lakini sasa inuka usimame wima. Nimekutokea kusudi nikuweke kuwa mutumishi wangu. Wewe utatoa ushuhuda juu yangu; utawaelezea watu mambo uliyoona leo na yale nitakayokuonyesha nyuma. Nitakuokoa toka mikono ya taifa lako la Waisraeli na ya watu wa mataifa mengine. Ninakutuma kwao kusudi ufungue macho yao, ukiwaongoza watoke katika giza na kuwaingiza katika mwangaza. Watatoka chini ya uwezo wa Shetani na kumugeukia Mungu, kusudi kwa njia ya kuniamini wapate kusamehewa zambi zao na kupewa urizi pamoja na watu wake watakatifu.’ “Kwa sababu hii, Ee mufalme Agripa, mimi nikafanya sawa nilivyoagizwa katika maono yale yaliyotoka mbinguni. Lakini kwanza nilihubiri wakaaji wa Damasiki, na wa Yerusalema na wa jimbo lote la Yudea nao watu wa mataifa mengine vilevile. Nilihubiri kwao kwamba wageuke toka zambi zao na kumurudilia Mungu, nao waonyeshe kwa njia ya matendo yao kwamba wamegeuka. Ni kwa sababu ya maneno hayo Wayuda walinikamata ndani ya hekalu na kutaka kuniua. Lakini kwa ulinzi wa Mungu ningali muzima hata leo. Nami ninatoa ushuhuda kwa wadogo na wakubwa, wala sisemi maneno mengine yanayokuwa mbali na yale manabii na Musa waliyosema kwamba yatatokea. Wao walitangaza kwamba Kristo anapaswa kuteswa na kuwa wa kwanza kufufuka kati ya wote waliokufa, naye atahubiri kwa Wayuda na kwa watu wa mataifa mengine kwamba kwa njia ya kuokolewa wataweza kuishi katika mwangaza.” Paulo alipokuwa akijitetea vile, Festo akamwambia kwa sauti kubwa: “Wewe Paulo, uko na wazimu! Elimu yako nyingi imekuvuruga kichwa.” Paulo akamujibu: “Muheshimiwa Festo, mimi si mwenda-wazimu. Maneno ninayosema ni ya kweli nayo ni ya maana. Mufalme Agripa anajua vizuri mambo yale yaliyotokea. Nami ninaweza kusema mbele yake pasipo woga kwa maana ninajua hakika kwamba hakuna hata jambo kati ya hayo asilofahamu, kwa sababu hayakufanyika kwa uficho. Ee Mufalme Agripa, unaamini maneno manabii waliyosema? Ninajua kama unayaamini!” Naye Agripa akamwambia Paulo: “Unazani kwamba kwa wakati kidogo utaweza kunivuta kuwa mukristo?” Paulo akajibu: “Ikiwa wakati kidogo au wakati murefu, ninamwomba Mungu, si juu yako wewe mwenyewe tu, lakini hata hawa wote wanaonisikiliza leo wapate kuwa sawa mimi, lakini wasifikie tu kutiwa katika kifungo!” Halafu mufalme, liwali, Berenike na wote wengine walioikaa pamoja nao wakasimama. Nao walipokwisha kuondoka wakasemezana: “Mutu huyu hakutenda neno linalomupasa kuuawa wala kufungwa.” Agripa akamwambia Festo: “Mutu huyu angeweza kufunguliwa, kama isingekuwa ameomba maneno yake yakatwe na Mufalme wa Roma.” Walipokwisha kukamata mupango wa kutusafirisha kwa njia ya chombo mpaka Italia, wakamuweka Paulo na wafungwa wengine chini ya uangalizi wa mukubwa mumoja wa waaskari aliyeitwa Yulio. Yeye alikuwa wa kundi la waaskari lililoitwa “Kundi la waaskari wa mufalme.” Tukapanda ndani ya chombo kilichotoka Adramiti, kilichokuwa tayari kupitia kwenye vivuko vya jimbo la Azia. Halafu tukaondoka tukiwa pamoja na mwanainchi mumoja wa Makedonia aliyeitwa Aristarko, wa Tesalonika. Kesho yake tukatua Sidona. Yulio aliyemutendea Paulo mema, akamupa ruhusa ya kwenda kuonana na warafiki zake, wapate kumupa vitu alivyohitaji. Kutoka kule, tukapita pembenipembeni ya kisanga cha Kipuro kwa kuepuka upepo uliokuwa ukivuma tokea mbele yetu. Tukavuka bahari upande wa jimbo la Kilikia na Pamfilia, na kufika katika muji Mira, wa jimbo la Likia. Kule yule mukubwa wa waaskari akakuta chombo kilichotoka Alesanduria kwa kwenda Italia, naye akatupandisha ndani yake. Tukasafiri polepole muda wa siku nyingi na kwa shida sana tukafika karibu na muji Kinido. Na kwa sababu upepo ulituzuiza kuendelea mbali ngambo ile, tukapita upande wa kusini wa kisanga cha Krete, kuelekea Salmone. Tuliendelea pembenipembeni yake kwa shida sana hata tukafika pahali panapoitwa “Vivuko Vizuri,” karibu na muji Lasea. Kisha kupitisha siku nyingi, tukafikia katika nyakati za hatari za safari ya bahari, kwa maana siku ya kufunga kula ilikuwa imekwisha kupita. Halafu Paulo akatupatia shauri hili: “Wanaume, ninaona kwamba safari yetu itakuwa ya hatari na hasara nyingi, si kwa chombo na mizigo tu, lakini kwa maisha yetu vilevile.” Lakini yule mukubwa wa waaskari akasadiki zaidi maneno ya kapiteni na ya mwenye chombo kuliko kufuata shauri la Paulo. Na kwa sababu kivuko kile hakikukuwa na nafasi zuri ya kukaa wakati wa baridi kali, watu wengi kati yetu wakakubaliana kuondoka kule, kusudi ikiwezekana wafike Foinike, na kupitishia wakati wa baridi kali kule. Foinike ni kivuko kimoja kinachokuwa katika kisanga cha Krete, kinachoelekea upande wa kaskazini-magaribi na wa kusini-magaribi. Upepo usiokuwa mukali ulipoanza kuvuma tokea kusini, wakazani kwamba wataweza tu kutimiza sawa walivyokuwa wamekusudia. Wakapandisha nanga na kuendelea pembenipembeni karibu sana na Krete. Lakini nyuma kidogo, upepo mukali sana wa zoruba unaotokea upande wa mashariki-kaskazini ukavuma ukishuka tokea kwenye kisanga. Upepo ukapeleka chombo, nacho hakikuweza kushindana nao. Halafu tukakiacha tu kipelekwe na upepo. Tulipokuwa tukipita upande wa kusini wa kisanga kidogo kinachoitwa Kauda, tuliweza kwa shida sana kuopoa mutumbwi unaokokotwa na chombo. Watumishi wa chombo walipokwisha kunyanyulia mutumbwi ule ndani ya chombo, wakakaza chombo kwa kukifungafunga na kamba kwa kukikingia na nguvu ya upepo. Na kwa kuwa waliogopa kwamba wasikwame kwenye lundo la muchanga wa ngambo ya Sirti, wakashusha tanga na kuachilia chombo kipelekwe na upepo. Kesho yake kwa kuona jinsi zoruba ilivyoendelea kutusukumasukuma kwa nguvu, wakaanza kutupa mizigo katika bahari. Na siku iliyofuata wakaamua kutupa hata vifaa vya chombo. Kwa muda wa siku nyingi hatukuweza kuona tena jua wala nyota, nayo zoruba ikaendelea kuvuma kwa nguvu. Kwa mwisho tukakata kitumaini chote cha kupona. Watu walikuwa wamepitisha siku nyingi bila kula kitu. Halafu Paulo akasimama mbele yao na kusema: “Warafiki zangu, mungefuata shauri langu na kutoondoka Krete, hamungepata hasara hii na kupoteza vitu kama hivi. Sasa ninawaomba mujipe moyo, kwa maana hakuna hata mumoja kati yenu atakayekufa, chombo tu ndicho kitakachoharibika. Kwa maana usiku malaika wa Mungu, ninayekuwa mutu wake na ninayemwabudu, alinitokea na kuniambia: ‘Paulo, usiogope! Sherti usambe mbele ya Mufalme wa Roma. Na tena kwa kuwa inamupendeza Mungu kukutendea mema, yeye ataokoa maisha ya watu hawa wote wanaosafiri pamoja nawe.’ Basi mujipe moyo, kwa sababu ninamutumainia Mungu kwamba itatendeka sawasawa nilivyoambiwa. Lakini ni sherti tutupwe kwenye kisanga kimoja.” Tulieneza majuma mawili tukipelekwa huku na huko na zoruba katika bahari ya Adria. Katikati ya usiku watumishi wa chombo waliwazia kwamba tumekaribia inchi kavu. Wakashusha kipimo ndani ya maji nao wakapata metre makumi ine kwenda chini. Mbali kidogo wakatupa tena kipimo na kupata metre makumi tatu. Kwa kuogopa kwamba chombo kisikwame kwenye mawe, wakashusha nanga ine za upande wa nyuma wa chombo na kungojea usiku ukuche. Wabaharia walitafuta kukimbia toka ndani ya chombo, wakashusha mutumbwi katika bahari, wakisema kwamba wanataka kufunga nanga tokea upande wa mbele. Lakini Paulo akamwambia yule mukubwa wa jeshi pamoja na waaskari wengine: “Watu hawa wasipobakia ndani ya chombo hamutaokolewa.” Halafu waaskari wakakata kamba zilizofunga ule mutumbwi na kuachilia uanguke katika bahari. Usiku ulipokaribia kucha, Paulo akawasihi watu wote kula chakula, akisema: “Sasa leo ni siku ya kumi na ine tangu mulipobaki bila kula kitu chochote. Basi ninawasihi ninyi mukule chakula, kwa sababu kitawafalia kusudi musikufe. Kwa maana hakuna mumoja kati yenu atakayepatwa na hasara yoyote hata kidogo.” Kisha kusema maneno hayo, Paulo akatwaa mukate, akamushukuru Mungu mbele yao wote, akaumega, na akaanza kula. Halafu wote wakatiwa moyo tena, nao vilevile wakakula chakula. Kwa jumla tulikuwa watu mia mbili na makumi saba na sita ndani ya chombo. Walipokwisha kushiba, wakatupa mizigo ya ngano katika bahari kwa kupunguza uzito wa chombo. Kulipokucha wabaharia hawakutambua inchi ile lakini wakaona nafasi bahari inapoingia ndani ya inchi kavu na kwenye kivuko. Basi wakakusudia kwenda kukwamisha chombo kule, kama ikiwezekana. Wakafungua nanga na kuziachilia zizame ndani ya bahari. Vilevile waliregeza kamba za makasia ya kuongoza chombo. Kisha wakafunga tanga ndogo mbele ya chombo kusudi kipelekwe na upepo, nao wakaelekea kwenye kile kivuko. Lakini wakakwama kwenye lundo ya muchanga na chombo kikakwama pale. Sehemu ya mbele ya chombo ikazama kabisa pasipo kutikisika, lakini sehemu ya nyuma ikavunjikavunjika kwa kupigwa na zoruba kwa nguvu. Halafu waaskari wakapata wazo la kuwaua wafungwa, kusudi hata mutu mumoja kati yao asitoroke kwa kuogelea. Lakini kwa kuwa mukubwa wa jeshi alitaka kumuponyesha Paulo, yeye akawazuiza wasitimize kusudi lao. Akaamuru wale waliojua kuogelea wajitupe wa kwanza ndani ya maji na kuvuka mpaka inchi kavu. Nao wengine wawafuate wakikamatilia kwenye mbao au kwenye vipande vya chombo. Ni vile watu wote walivyofika inchi kavu salama. Tulipokwisha kuponyoka kufa, ndio wakati tulijua kwamba kisanga kile tulichokuwa ndani yake kinaitwa Melita. Wenyeji wa kule wakatutendea mema sana. Mvua ilikuwa imeanza kunyesha na kulikuwa baridi, kwa hiyo watu wale wakatukongea moto na kutukaribisha sisi wote. Paulo akatwaa lundo ya kuni, na alipokuwa akiiweka ndani ya moto, nyoka akatoka katikati ya ile lundo kwa sababu ya kivukuto na kujizingia kwa mukono wake. Wale wenyeji wa kule walipoona nyoka yule anajizingia kwa mukono wake wakasemezana: “Hakika mutu huyu ni mwuaji, kwa maana ijapokuwa alipona katika hatari ya bahari, kufuatana na azabu ya haki ya Mungu, kufa kwake kunatimia.” Lakini Paulo akamukungutia yule nyoka katika moto wala hakumuzuru hata kidogo. Nao watu wale walingojea kuona ikiwa atavimba mukono au ataanguka mara moja na kufa. Lakini kisha kungoja muda murefu na kuona kwamba hakupata hasara yoyote, wakabadilisha mawazo yao hata wakasema kwamba yeye ni mumoja wa miungu. Karibu na pale kulikuwa mashamba ya mukubwa wa kisanga, aliyeitwa Publio. Mutu yule akatukaribisha kwa upendo na kutupangisha ndani ya nyumba yake kwa muda wa siku tatu. Baba ya Publio alikuwa amelala kwa ajili ya kuwezwa na ugonjwa wa homa na wa kuhara damu. Paulo akaenda kumwangalia, akamwombea na kuweka mikono juu yake, naye akapona. Na kufuatana na jambo hilo, wagonjwa wengine waliokaa katika kisanga kile wakakuja, nao wakaponyeshwa vilevile. Watu wakatuheshimu sana, na wakati tulipoondoka kwa njia ya chombo kwa kuendelea wakatupatia vitu vyote tulivyohitaji kwa safari yetu. Kulipopita miezi mitatu, tukasafiri katika chombo kimoja kilichobaki katika kisanga kile kwa kungojea wakati wa baridi kali upite kwanza. Chombo kile kilikuwa chenye kutoka Alesanduria. Na juu yake kulikuwa michoro ya sanamu za mapacha ya miungu. Tulipofika Sirakuse, tukakaa kule kwa muda wa siku tatu. Kutoka kule tukazunguka pembenipembeni ya bahari hata tukafika katika muji Regio. Kesho yake upepo usiokuwa mukali ukaanza kuvuma tokea kusini, na kwa mwendo wa siku mbili tukafika katika muji Puteoli. Kule tukakuta wandugu waamini, nao wakatualika tukae pamoja nao kwa muda wa juma moja. Ni vile tulivyosafiri hata kufika Roma. Wandugu waamini wa Roma waliposikia habari zetu wakakuja kutuona kwenye Soko la Apio na wengine kwenye Tiretaberne. Paulo alipowaona, akamushukuru Mungu na kutiwa tena moyo. Tulipofika Roma, Paulo akapewa ruhusa ya kujilipia nyumba ya kupanga ambamo atakaa pamoja na askari mumoja mwenye kumuchunga. Kulipopita siku tatu, Paulo aliwaita wakubwa wa Wayuda waliokaa kule. Na walipokwisha kukusanyika akawaambia: “Wandugu, mimi nilifungwa kule Yerusalema na kutolewa kwa Waroma ijapokuwa sikufanya kosa lolote juu ya taifa letu wala kuvunja desturi za babu zetu. Nao walipokwisha kunisambisha, walitaka kunifungua kwa sababu hawakuniona na kosa linalonipasa kuuawa. Lakini nilipoona kwamba Wayuda wanakataa shauri lile, ilinilazimisha kuomba nisambishwe na Mufalme wa Roma. Na katika haya yote sikukuwa na mashitaki yoyote juu ya taifa langu. Basi ni kwa sababu hii nimewaita kusudi tuonane na niseme nanyi, kwa maana ninafungwa na munyororo huu kwa ajili ya tumaini ambalo Waisraeli wanakuwa nalo.” Wakamwambia: “Sisi hatukupokea barua juu yako toka Yudea, wala ndugu Muyuda aliyefika huku kwa kutupasha habari, wala kusema ubaya juu yako. Lakini tungependa kusikia mawazo yako kwa maana tunajua kwamba fasi zote watu wanapinga dini hii unayofuata.” Halafu wakapanga siku ya kukutana na Paulo. Na siku ile watu wengi zaidi wakamufikia pahali alipopanga. Na tangu asubui mpaka magaribi Paulo akawaelezea mambo mengi na kutoa ushuhuda juu ya habari za Ufalme wa Mungu. Alitaka wasadiki habari za Yesu akitaja maneno ya Sheria ya Musa na ya vitabu vya manabii. Wamoja wakasadiki maneno yaliyosemwa, lakini wengine hawakuyaamini. Nao walipokuwa wakiondoka bila kupatana, Paulo akaongeza kuwaambia maneno haya tu: “Roho Mutakatifu alikuwa na sheria ya kusema hivi kwa babu zenu kwa njia ya nabii Isaya: Uwaendee watu hawa na kuwaambia: Kusikia mutasikia, lakini hamutafahamu. Kuangalia mutaangalia, lakini hamutatambua. Maana mioyo ya watu hawa imegeuka kuwa migumu, wameziba masikio yao na wamefunga macho yao. Isingekuwa hivi, wangeona na macho yao, wangesikia na masikio yao, wangefahamu na mioyo yao, na wangegeukia kwangu na ningewaponyesha. “Na kwa kumaliza, basi mujue kwamba habari ya wokovu huu wa Mungu imetumwa kutangazwa kwa watu wa mataifa mengine, nao wataisikia!” [ Paulo alipokwisha kusema maneno haya, Wayuda wakaenda wakibishana sana wao kwa wao.] Paulo akakaa miaka miwili katika nyumba aliyokuwa akijilipia yeye mwenyewe. Alikaribisha watu wote waliokuja kumwona. Alihubiri habari za Ufalme wa Mungu na kuwafundisha watu juu ya Bwana Yesu Kristo bila woga na bila kuzuizwa. Barua hii inatoka kwangu mimi Paulo, mutumishi wa Kristo Yesu, niliyeitwa na Mungu kuwa mutume na niliyewekwa kwa kazi ya kutangaza Habari Njema yake. Habari Njema hiyo iliahidiwa na Mungu tangu zamani kwa kinywa cha manabii wake katika Maandiko Matakatifu. Kwa njia yake Mungu amenipa neema ya kuwa mutume kusudi niongoze mataifa yote yapate kumwamini na kumutii. Na kwa tendo hilo jina lake lipate kusifiwa. Nanyi vilevile munakuwa kati ya watu wale; mumeitwa na Mungu mukuwe watu wa Yesu Kristo. Ninawaandikia ninyi wote wapenzi wa Mungu munaokaa Roma, mulioitwa kuwa watu wake watakatifu. Ninawatakia neema na amani kutoka kwa Mungu Baba yetu na kwa Bwana Yesu Kristo. Kwanza ninamushukuru Mungu wangu kwa njia ya Yesu Kristo kwa ajili yenu ninyi wote, kwa sababu habari za imani yenu zinasambaa katika dunia nzima. Mungu ambaye ninamwabudu kwa roho yangu yote kwa njia ya kutangaza Habari Njema ya Mwana wake, ni mushuhuda wangu kwamba ninawakumbuka siku zote katika maombi yangu. Ninaomba kwamba Mungu akitaka, anifungulie njia ya kuwatembelea siku hizi. Kwa maana ninatamani sana kuonana nanyi, kusudi nigawanye pamoja nanyi zawadi ya kiroho, mupate kusimama imara. Ni kusema kwamba nipate kutiwa moyo kwa njia ya imani yenu na ninyi kwa njia ya imani yangu. Wandugu zangu, ninataka mujue kwamba mara nyingi nilikusudia kuwatembelea, lakini mpaka sasa ninapata vizuizo. Ningetamani kupata matunda ya kazi yangu katikati yenu vilevile, kama inavyokuwa katikati ya watu wa mataifa mengine. Kwa sababu ninapaswa kwanza kuwaendea watu wote: Wagriki na wasiokuwa Wagriki, wenye elimu na wasiokuwa na elimu. Ni kwa sababu hii ninatamani sana kuhubiri vilevile Habari Njema kwenu ninyi munaokaa Roma. Mimi sisikii haya juu ya Habari Njema, kwa sababu huo ndio uwezo wa Mungu unaowaokoa wote wanaoamini, kwanza Wayuda na kisha watu wa mataifa mengine vilevile. Kwa maana Habari Njema inaonyesha namna Mungu anavyowahesabia watu haki mbele yake. Jambo hilo haliwezekani isipokuwa kwa njia ya kuamini tu. Ni sawa vile inavyoandikwa katika Maandiko Matakatifu yanayosema: “Mwenye haki ataishi kwa njia ya imani.” Tokea mbinguni Mungu anaonyesha kwamba anawakasirikia wote wanaofanya zambi na maovu, wanaowazuiza watu wasitambue ukweli kwa njia ya matendo yao mabaya. Kwa maana mambo yanayoweza kujulikana juu ya Mungu ni wazi kwao, kwa kuwa Mungu mwenyewe ameyaonyesha kwao waziwazi. Tangu Mungu alipoumba dunia, hali zake zisizoonekana, ni kusema uwezo wake wa milele na umungu wake, vinaonekana kupitia viumbe vyake. Kwa sababu hii watu wale hawatapata namna yoyote ya kujitetea. Ijapokuwa wanamujua Mungu, hawamutukuzi wala kumushukuru kama vile anavyostahili. Lakini mawazo yao yaligeukia mambo ya ovyo ovyo, na mioyo yao isiyokuwa na ufahamu ilibaki katika giza. Wanajidai kwamba wao ni wenye hekima, lakini wako wapumbafu. Kwa pahali pa kumwabudu Mungu anayeishi milele, wakaabudu sanamu zilizochongwa kwa mufano wa mutu anayekufa, wa ndege, wa nyama na hata viumbe vyenye kutambaa. Kwa sababu hii Mungu aliwaacha wajichafue wenyewe kwa kufuata tamaa ya mioyo yao na kutendeana mambo ya haya wao kwa wao. Wanabadilisha ukweli juu ya Mungu kuwa uongo; wanaabudu na kutumikia vitu vilivyoumbwa kuliko Muumba mwenyewe, anayestahili kutukuzwa milele! Amina. Kwa hiyo Mungu aliwaacha wafuate tamaa zao za haya. Wanawake wao wanabadilisha matumizi ya kawaida na matumizi isiyokuwa ya kawaida. Na wanaume nao vilevile wanabadilisha matumizi ya kawaida ya mume na muke, wakiwakiana tamaa wanaume kwa wanaume. Kwa ajili ya hiyo, wanajipatia wenyewe azabu wanayoistahili kufuatana na huo upotevu wao. Hivi kufuatana na vile walivyokataa kumutambua Mungu, Mungu akawaacha wafuate akili yao ya upotevu, kusudi wafanye mambo wasiyopaswa kufanya. Wamejaa kila namna ya uovu, ubaya, tamaa na upotovu. Wamejaa wivu, uuaji, ugomvi, udanganyifu na ukorofi. Wao ni wenye kuchongeana, wasingiziaji, wenye kumuchukia Mungu, wenye kasirani, wenye kiburi na wenye kujivuna. Wao ni werevu kwa kutenda mabaya, hawatii wazazi wao, hawana zamiri, hawawezi kuaminiwa, hawana upendo wala huruma. Nao wanajua kwamba Sheria ya Mungu inasema kwamba watu wanaotenda maneno haya wanastahili kufa. Lakini hata hivi wanaendelea, si kuyafanya tu, lakini kukubaliana na wale wanaoyatenda. Wewe unayemuhukumu mwingine hauna namna yoyote ya kujitetea, haizuru wewe ni nani. Kwa maana wakati unapohukumu mwingine, unajikatia hukumu wewe mwenyewe, kwa sababu wewe unayehukumu unatenda mambo yale yale. Tunajua kwamba Mungu anahukumu kwa haki watu wanaofanya mambo ya namna hiyo. Basi wewe unawahukumu wale wanaofanya mambo yale, lakini wewe mwenyewe unayafanya! Unafikiri kwamba utaponyoka hukumu ya Mungu? Au haujali na uwingi wa wema, utulivu na uvumilivu wa Mungu? Haujui kwamba wema wake ungeweza kukuongoza hata upate kugeuka toka zambi? Lakini wewe ni mugumu na mwenye moyo usiotaka kugeuka. Kwa hiyo unajiwekea azabu kubwa siku Mungu atakapoonyesha kasirani yake na hukumu yake ya haki. Kwa maana Mungu atamulipa kila mutu kwa kadiri ya matendo yake. Wale wanaofanya matendo mema bila kuchoka na kutafuta toka kwa Mungu utukufu, heshima na uzima usiokuwa na mwisho, Mungu atawapa uzima wa milele. Lakini wapingaji na wale wanaokataa kufuata ukweli, wakifuata uovu, wataangukiwa na kasirani na hasira ya Mungu. Mateso na taabu zitamupata kila mutu anayefanya mabaya: kwanza Wayuda, kisha watu wa mataifa mengine vilevile. Lakini kila mutu anayefanya mema atapata utukufu, heshima na amani; kwanza Wayuda, kisha watu wa mataifa mengine vilevile. Kwa maana Mungu hana upendeleo. Wote wanaofanya zambi pasipo kujua Sheria ya Musa watapotea pasipo kuhukumiwa na Sheria ile. Lakini wote wanaofanya zambi wakijua Sheria watahukumiwa kufuatana na Sheria. Ni vile kwa sababu si wale wanaosikia Sheria ndio wanaohesabiwa haki mbele ya Mungu, lakini ni wale wanaotii Sheria. Watu wa mataifa hawana Sheria ya Musa. Lakini wanapofanya sawa inavyoamuriwa na Sheria ile kutokana na zamiri yao, wao ni Sheria kwa ajili yao wenyewe, ijapokuwa hawana Sheria ile. Kwa maana wanaonyesha kwamba maagizo ya Sheria yameandikwa ndani ya mioyo yao. Zamiri yao vilevile inawahukumu, na mawazo yao yenyewe yanawashitaki au yanawatetea. Hiyo ndiyo itakayotokea siku ile Mungu atakapohukumu mambo ya siri ya watu kwa njia ya Yesu Kristo, kama vile Habari Njema yangu inavyosema. Sasa wewe unaitwa Muyuda, unategemea Sheria na kujivunia Mungu. Unajidai kwamba unajua mapenzi yake na kutambua mambo yanayofaa zaidi kwa sababu umefundishwa na Sheria. Unajiaminia kwamba wewe ni mwongozi wa vipofu na mwangaza kwa wale wanaokuwa katika giza, mufundisha wajinga na mwalimu wa watoto, kwa sababu kutokana na Sheria unajua uhakika juu ya mambo ya elimu na ya kweli. Basi wewe unayewafundisha watu wengine, kwa sababu gani haujifundishi wewe mwenyewe? Wewe unayehubiri kwamba haifai kuiba, kwa nini unaiba? Wewe unayesema kwamba haifai kuzini, kwa nini unazini? Wewe unayechukia sanamu za miungu, kwa nini unaiba vitu ndani ya hekalu zao? Unajisifu kwamba unajua Sheria, lakini unamuzarau Mungu kwa kuvunja Sheria! Kwa maana kama ilivyoandikwa katika Maandiko Matakatifu: “Kwa sababu yenu, jina la Mungu linatukaniwa katikati ya watu wa mataifa mengine.” Kutahiriwa kuna mafaa kama ukitii Sheria. Lakini usipotii Sheria, wewe unahesabiwa kama mutu asiyetahiriwa. Na kama mutu asiyetahiriwa akitii maagizo ya Sheria, Mungu hatamuhesabu kuwa ametahiriwa? Mutu asiyetahiriwa kimwili, lakini anatii Sheria, atakuhukumu wewe unayevunja Sheria ijapokuwa unajua maandiko ya Sheria na umetahiriwa. Kwa maana kuonekana kwa inje kwa Muyuda si kuwa Muyuda wa kweli, wala kutahiriwa kimwili tu si kutahiriwa kwa kweli. Lakini Muyuda wa kweli ni yule anayekuwa Muyuda kwa ndani, nako kutahiriwa kwa kweli ni kule Roho Mutakatifu anakofanya ndani ya moyo wa mutu, wala si kule kunakofanyika kwa njia ya maandiko ya Sheria. Mutu wa namna hii hapati sifa kutoka kwa watu lakini kutoka kwa Mungu. Basi kuna faida gani kuwa Muyuda? Na kutahiriwa kuna mafaa gani? Kuna faida kubwa sana kila upande. Kwanza, Mungu alifunua Neno lake kwa Wayuda kusudi walishike. Tuseme nini basi? Ikiwa wamoja kati yao hawakukuwa waaminifu, jambo hilo litaweza kuonyesha kwamba Mungu ataacha kuwa mwaminifu? Hapana hata kidogo! Sherti Mungu ajulikane kuwa mwenye ukweli, na kila mutu kuwa mwongo, kama inavyoandikwa katika Maandiko Matakatifu: “Ee Mungu, sherti ujulikane kuwa mwenye haki katika masemi yako. Nawe ushinde wakati unaposhitakiwa.” Lakini ikiwa kwa njia ya ubaya tunaofanya, Mungu anaonekana kuwa mwenye haki, basi tutasema kama Mungu hana haki wakati anapotuazibu? (Ninasema kwa mafikiri ya kimutu.) Hapana hata kidogo! Ingekuwa vile, namna gani basi Mungu angeweza kuhukumu dunia? Lakini ikiwa kwa njia ya uongo wangu ukweli wa Mungu unaonekana naye anatukuzwa zaidi, basi kwa nini tena ninahukumiwa kama mwenye zambi? Ikiwa ni vile, basi tuseme: “Tufanye mabaya kusudi kutokee mema”? Hakika kuna watu wamoja wanaonisingizia wakisema kwamba nimesema vile. Watu hawa wataazibiwa sawa inavyowapasa! Basi tuseme nini? Sisi Wayuda tunawapita watu wa mataifa mengine nini? Hatuwapiti kitu hata kimoja! Kwa maana nimekwisha kuonyesha kwamba Wayuda na watu wa mataifa mengine wote wako chini ya utawala wa zambi. Ni sawa ilivyoandikwa katika Maandiko Matakatifu: “Hakuna hata mutu mumoja mwenye haki! Hakuna mutu mwenye ufahamu, hakuna mwenye kushugulika na Mungu. Wote wamepotea, wote kwa jumla wamepotoka. Hakuna mwenye kufanya mema, hata mumoja. Vinywa vyao ni kama kaburi wazi, ndimi zao ni za kudanganya, ndani ya midomo yao munatoka sumu kali sawa ya nyoka. Vinywa vyao vinajaa laana na maneno ya uchungu. Wao ni wepesi kwa kumwanga damu. Wanaharibu na kuangamiza popote wanapopita, hawawazi juu ya njia ya kuleta amani, nao hawamwogopi Mungu hata kidogo.” Basi tunajua kama maneno yote yanayosemwa na Sheria, yanawaelekea wale wanaolazimishwa kutii Sheria, kusudi mutu yeyote asikuwe na namna ya kujitetea, na dunia nzima ipaswe kuhukumiwa na Mungu. Kwa sababu hakuna mutu atakayehesabiwa haki mbele ya Mungu kwa kuwa anatii Sheria, maana Sheria inamusaidia mutu tu kwa kutambua kwamba amefanya zambi. Lakini sasa Mungu ameonyesha njia ya kumuhesabia mutu haki mbele yake, na si kwa njia ya Sheria. Maandiko ya Sheria na manabii yanashuhudia kwamba kuhesabiwa haki na Mungu kunapatikana kwa njia ya imani katika Yesu Kristo kwa wote wanaoamini, kwa maana hakuna tofauti yoyote kati yao, kwa maana wote wamefanya zambi na kukosa utukufu wa Mungu. Lakini kwa neema ya Mungu wanahesabiwa haki kwa bure kwa njia ya Kristo Yesu anayewakomboa. Basi sasa mutu ataweza kujivuna? Hapana! Kwa sababu gani? Kwa sababu anatii Sheria? Hapana. Lakini kwa sababu anamwamini Yesu. Kwa maana tunaona kama mutu anahesabiwa haki mbele ya Mungu kwa njia ya imani wala si kwa njia ya kutii Sheria. Au Mungu ni Mungu wa Wayuda tu? Yeye si Mungu wa watu wa mataifa mengine vilevile? Ndiyo, yeye ni Mungu wa watu wa mataifa mengine vilevile, kwa sababu kuna Mungu mumoja tu. Na ni yeye atakayewahesabia Wayuda na watu wa mataifa mengine haki mbele yake kwa njia ya imani ya kila wamoja. Basi ni kusema kwa sababu ya imani ile tunaitupilia Sheria? Hapana hata kidogo! Lakini tunasimamisha Sheria. Basi tuseme nini juu ya babu yetu Abrahamu? Nini iliyomutokea? Ikiwa Abrahamu alihesabiwa haki mbele ya Mungu kwa njia ya matendo yake, angeweza kujivuna. Lakini hawezi kujivuna mbele ya Mungu. Kwa maana Maandiko Matakatifu yanasema: “Abrahamu alimwamini Mungu na kwa hiyo akahesabiwa kuwa mwenye haki.” Mutu anayefanya kazi, mushahara wake hauhesabiwi kama zawadi, lakini ni haki yake. Lakini mutu asipotegemea matendo yake mwenyewe, naye akimwamini Mungu anayemuhesabia mwovu haki, basi imani yake inahesabiwa kuwa haki. Na ni vile Daudi anavyosema juu ya uheri wa mutu ambaye Mungu anayehesabia haki pasipo kuangalia matendo yake. “Heri wale waliosamehewa makosa yao, nazo zambi zao zimefutwa. Heri mutu yule Bwana asiyemuhesabia zambi zake.” Uheri huu si kwa watu wanaotahiriwa tu, lakini ni kwa watu wasiotahiriwa vilevile. Kwa maana tumekwisha kusema kwamba Abrahamu alihesabiwa kuwa mwenye haki kwa njia ya imani yake. Yeye alihesabiwa vile alipokuwa katika hali gani? Alipokuwa amekwisha kutahiriwa au alipokuwa hajatahiriwa bado? Halikutendeka nyuma ya kutahiriwa kwa Abrahamu lakini mbele ya kutahiriwa kwake! Nyuma ya pale alitahiriwa, na kutahiriwa kwake kulikuwa kitambulisho cha kuhakikisha ile haki Mungu aliyomuhesabia kwa njia ya imani yake. Hivi Abrahamu akakuwa baba wa watu wote wanaoamini, ijapokuwa hawatahiriwi, kusudi wao vilevile wahesabiwe haki. Vilevile yeye ni baba ya wale wanaotahiriwa, si kwa sababu wametahiriwa tu, lakini kwa sababu wanafuata vilevile njia ile ile ya imani ambayo babu yetu Abrahamu alifuata alipokuwa hajatahiriwa. Mungu alimwahidi Abrahamu na wazao wake kwamba atawapa dunia kuwa urizi wao, si kwa sababu alishika Sheria lakini kwa sababu Mungu alimuhesabia haki kwa njia ya imani yake. Kwa maana ikiwa wale wanaotii Sheria ndio watakaopokea kitu anachoahidi, basi imani haina mafaa yoyote, nayo ahadi ya Mungu ni bure. Kwa sababu Sheria inaamusha kasirani ya Mungu. Lakini Sheria haingekuwa, kuvunja Sheria hakungekuwa vilevile. Kwa hiyo ahadi inafuatana na imani, kusudi ikuwe imetolewa kwa neema ya Mungu. Na zaidi kuwe uhakikisho kwamba ahadi hiyo ni kwa ajili ya wazao wote wa Abrahamu, si kwa wale wanaotii Sheria tu, lakini vilevile kwa wale wanaokuwa na imani kama Abrahamu, babu yetu sisi wote. Ni sawa vile inavyoandikwa katika Maandiko Matakatifu: “Nimekuweka kuwa babu wa mataifa mengi.” Abrahamu alimwamini Mungu, kwa hiyo yeye ni baba yetu mbele yake. Ni yeye Mungu anayewafufua wafu na kuamuru vitu visivyokuwa vipate kuwa. Abrahamu aliamini na kutumainia mambo ambayo yasingewezekana kutumainia na hivi akakuwa babu ya mataifa mengi, kufuatana na maneno haya Mungu aliyomwambia: “Hivi ndivyo wazao wako watakavyokuwa wengi.” Yeye alikuwa na umri wa miaka karibu mia moja, lakini imani yake haikupunguka alipofikiri juu ya hali yake iliyokuwa kama ya mwenye kungojea tu lufu wala juu ya hali ya Sara aliyekuwa hawezi tena kuzaa. Hakuona shaka juu ya ahadi aliyopewa na Mungu wala kupoteza tumaini, lakini imani yake ilimutia nguvu hata akamutukuza Mungu. Alifanya vile kwa sababu alijua hakika kwamba yule aliyetoa ahadi ile yuko na uwezo wa kuitimiza. Kwa sababu hiyo “alihesabiwa kuwa mwenye haki”. Lakini maneno hayo “alihesabiwa kuwa mwenye haki” hayakuandikwa kwa ajili yake yeye mwenyewe, lakini vilevile kwa ajili yetu sisi tutakaohesabiwa haki. Ndio sisi tunaomwamini yule aliyemufufua Yesu Bwana wetu. Alitolewa kufa sababu ya makosa yetu na kufufuliwa kusudi tupate kuhesabiwa haki mbele ya Mungu. Sasa kufuatana na vile tumekwisha kuhesabiwa haki mbele ya Mungu kwa njia ya imani, kunakuwa sasa amani kati yetu na Mungu kwa njia ya Bwana wetu Yesu Kristo. Kwa njia ya imani, Yesu ametuwezesha kukaribia neema ya Mungu, inayokuwa musingi wetu. Sababu hii tunafurahi tukiwa na tumaini la kushiriki katika utukufu wa Mungu. Zaidi ya hii, tunafurahi vilevile kwa ajili ya mateso tunayopata, kwa sababu tunajua kwamba mateso yanaleta uvumilivu, na uvumilivu unaleta uaminifu kamili na uaminifu ule unaleta tumaini. Nalo tumaini hili si la udanganyifu, kwa sababu Mungu amemimia upendo wake ndani ya mioyo yetu kwa njia ya Roho Mutakatifu aliyetupatia. Kwa maana tulipokuwa hatuna uwezo wowote, Kristo alikufa kwa ajili ya waovu kwa wakati uliopangwa. Ni vigumu kwa mutu kukubali kufa kwa ajili ya mwenye haki. Labda mutu anaweza kujitolea kufa kwa ajili ya mutu mwema. Lakini Mungu ameonyesha wazi upendo wake kwetu ni wapata gani, kwa maana tulipokuwa tungali wenye zambi, Kristo alikufa kwa ajili yetu. Sasa kwa kuwa tumehesabiwa haki mbele ya Mungu kwa njia ya damu ya Yesu, inaonyesha zaidi sana kwamba atatuokoa kusudi kasirani ya Mungu isituangukie. Basi ikiwa kama tulipokuwa waadui za Mungu tulipatanishwa naye kwa njia ya kufa kwa Mwana wake, inaonyesha zaidi sana kwamba tukiwa tumepatanishwa naye, tutaokolewa kwa njia ya uzima wa Kristo. Wala si ile tu, lakini tunafurahi kwa ajili ya Mungu kwa njia ya Bwana wetu Yesu Kristo aliyetupatanisha sasa na Mungu. Kwa njia ya mutu mumoja zambi iliingia katika dunia, nayo zambi ikaleta kifo. Ni hivi vilevile kifo kimefikia watu wote, kwa sababu wote wamefanya zambi. Kulikuwa zambi katika dunia mbele hakujakuwa Sheria, na kwa muda Sheria ilipokuwa haijakuwa, Mungu hakuhesabu zambi. Lakini kifo kilitawala tangia wakati wa Adamu mpaka wakati wa Musa, hata juu ya wale wasiofanya zambi kwa kuvunja amri, sawa vile Adamu alivyofanya. Naye ni mufano wa yule aliyengojewa kuja. Lakini kuna tofauti kubwa kati ya zawadi ya Mungu na kosa la Adamu. Kwa maana ikiwa kosa la mutu mumoja lilisababisha kifo cha watu wengi, inaonyesha zaidi sana kwamba Mungu amezidisha neema yake kwa ajili ya watu wengi na zawadi inayotokana nayo kwa njia ya mutu mumoja, Yesu Kristo. Tena, kuna tofauti kati ya zawadi ya Mungu na mambo yaliyotokea kwa sababu ya zambi ya yule mutu mumoja. Kwa maana hukumu iliyosababishwa na zambi ya mutu mumoja, ilileta azabu, lakini zawadi ya neema ambayo Mungu alitoa kisha makosa mengi, ilileta kuhesabiwa haki mbele yake. Ni kweli kwamba kifo kilitawala kwa njia ya mutu mumoja, kwa sababu ya kosa la huyo mumoja. Lakini inaonyesha zaidi sana kwamba wale wanaopewa neema ya Mungu kwa uwingi na zawadi ya haki yake, wataishi na kutawala kwa njia ya mutu mumoja, Yesu Kristo. Basi kama vile kosa la mutu mumoja limewaletea watu wote azabu, ni hivi vilevile tendo la haki la mutu mumoja limewaweka huru na kuwapa uzima. Na kama vile kutokana na uasi wa mutu mumoja, watu wengi wamekuwa wenye zambi, ni hivi vilevile kutokana na utii wa mutu mumoja, watu wengi watahesabiwa haki mbele ya Mungu. Sheria ilitokea na kusababisha kuongezeka kwa makosa, lakini nafasi yoyote palipozidi zambi, neema ilizidi sana. Hivi kama vile zambi ilivyotawala na kuleta kifo, hivi vilevile neema ya Mungu itawale kwa njia ya haki na kuleta uzima wa milele, kwa njia ya Yesu Kristo Bwana wetu. Basi sasa tuseme nini? Tuendelee kuishi katika zambi kusudi neema ya Mungu izidi kuongezeka? Hapana hata kidogo! Sisi tuliokufa kwa ajili ya zambi, namna gani tutaweza tena kuishi katika zambi? Munajua hakika kwamba sisi wote tulipobatizwa tuliungana na Yesu Kristo; kwa njia hiyo tuliungana naye katika kufa. Hivi, kwa njia ya ubatizo, tuliungana naye katika kufa na katika kuzikwa kwake, kusudi kama vile Kristo alivyofufuliwa kwa uwezo wenye utukufu wa Baba, sisi vilevile tupate kuishi katika maisha mapya. Ikiwa tuliungana naye kwa njia ya kufa kama yeye, tutaungana naye vilevile kwa njia ya kufufuliwa kama yeye. Kwa maana tunajua kwamba ule utu wetu wa zamani ulitundikwa pamoja na Kristo, kusudi tusitawaliwe tena na hiyo tabia ya zambi na tusikuwe tena watumwa wa zambi. Kwa sababu mutu akikufa anapata uhuru toka katika zambi. Ikiwa tumekufa pamoja na Kristo, tunaamini kwamba tutaishi pamoja naye vilevile. Kwa maana tunajua kwamba Kristo amefufuliwa, naye hawezi kufa tena, kwa sababu kifo hakina tena uwezo juu yake. Kuelekea jambo la kufa kwake, alikufa mara moja tu kwa ajili ya zambi; lakini kuelekea maisha yake, sasa anaishi kwa ajili ya Mungu. Hivi vilevile mujihesabu kuwa mumekufa kwa ajili ya zambi na kuwa munaishi pamoja na Mungu mukiungana na Yesu Kristo. Basi musiache tena zambi kutawala katika mwili wenu wa kufa, hata mupate kufuata tamaa zake mbaya. Musitoe tena viungo vya mwili wenu kufanya zambi, mukivitumikisha kama vyombo vya kufanya mabaya. Lakini mujitoe wenyewe kwa kumutumikia Mungu kama watu waliofufuliwa na mutumikishe viungo vya mwili wenu kama vyombo vya kufanya haki. Kwa maana hamutatawaliwa tena na zambi, kwa sababu hamuishi chini ya uongozi wa Sheria lakini chini ya uongozi wa neema ya Mungu. Ni nini basi? Tufanye zambi kwa sababu sisi hatuishi chini ya Sheria, lakini chini ya uwongozi wa neema ya Mungu? Hapana hata kidogo! Munajua hakika kwamba mukijitoa wenyewe kwa mutu fulani kuwa watumwa wake na kulazimishwa kumutii, munakuwa kweli watumwa wa yule munayemutii. Ikiwa ni utumwa wa zambi, mwisho wake ni kifo; ikiwa ni kumutii Mungu, mwisho wake ni maisha ya haki. Lakini asante kwa Mungu, kwa maana ninyi muliokuwa zamani watumwa wa zambi mumetii sasa kwa moyo wenu wote kanuni za mafundisho muliyopewa. Mumewekwa kuwa huru toka katika utumwa wa zambi, na sasa mumegeuka watumwa wa haki. (Ninatumia luga ya kawaida ya wanadamu kwa sababu ya uzaifu wenu wa kimutu). Zamani mulijitoa kabisa kuwa watumwa wa kufanya mambo machafu na maovu kwa kuishi katika machafuko. Hivi vilevile mujitoe kabisa kuwa watumwa wa kufanya haki kusudi muweze kuishi katika utakatifu. Wakati mulipokuwa watumwa wa zambi, mulikuwa huru kufuatana na mambo ya haki. Basi mulipata faida gani kwa kufanya mambo yale munayopata haya juu yake sasa? Maana mwisho yao ni kifo! Lakini sasa kufuatana na vile mumewekwa huru toka utawala wa zambi na kugeuka watumwa wa Mungu, munapata faida ya kuishi katika utakatifu na kwa mwisho kupewa uzima wa milele. Kwa maana mushahara wa zambi ni kifo, lakini zawadi Mungu anayotoa ni uzima wa milele kwa kuungana na Yesu Kristo, Bwana wetu. Wandugu zangu, munajua uhakika juu ya maneno haya nitakayowaambia, kwa maana ninyi ni watu wanaoelewa Sheria vizuri: Sheria haina mamlaka juu ya mutu isipokuwa tu wakati angali muzima. Kwa mufano, mwanamuke aliyeolewa anafungwa na Sheria katika maisha yake na mume wake wakati mume wake angali muzima. Lakini kama mume wake akikufa, yeye anakuwa huru kufuatana na Sheria ile iliyomufunga. Basi kama akiolewa na mutu mwingine wakati mume wake angali muzima, atahesabiwa kuwa muzinzi. Lakini kama mume wake akikufa, yeye anakuwa huru toka Sheria ile iliyomufunga na hata akiolewa na mutu mwingine hatahesabiwa kuwa muzinzi. Nanyi wandugu zangu, ni hivi inavyokuwa kwa ngambo yenu. Kufuatana na maneno ya Sheria, ninyi vilevile mumekufa, kwa maana muliungana na mwili wa Kristo. Na sasa munakuwa wa mutu mwingine, ndiye yule aliyefufuka, kusudi tupate kufanya matendo yanayofaa katika kazi ya Mungu. Kwa maana tulipoishi maisha ya kimwili, tamaa ya kufanya zambi iliyotokana na Sheria ilitumika ndani yetu na kutuletea kifo. Lakini sasa tumekuwa huru toka vifungo vya Sheria, kwa maana tunakuwa kama waliokufa kufuatana na mambo yale yaliyotufunga. Kwa hiyo tunaweza kumutumikia Mungu kwa kufuata njia mupya chini ya uongozi wa Roho wake, wala si kufuata njia ya zamani chini ya uongozi wa maandiko ya Sheria. Tuseme nini basi? Sheria ni zambi? Hapana hata kidogo! Lakini pasipo Sheria singejua zambi ni nini. Kwa maana singejua kutamani ni nini kama Sheria isingesema: “Usitamani.” Kutokana na amri, zambi ilipata njia hata kuamusha kila namna ya tamaa ndani yangu. Kwa maana pasipo Sheria zambi ingekuwa kama mufu. Zamani nilikuwa muzima pasipo kujua Sheria, lakini wakati amri ilipotokea, zambi ikaanza kutenda kazi, nami nikakufa. Hivi ile amri iliyopasa kuniletea uzima ikaniletea kifo. Maana kutokana na amri ile, zambi ilipata njia ya kunidanganya na kuniua kufuatana na amri ile ile. Basi Sheria yenyewe ni takatifu na amri ni takatifu, ya haki na nzuri. Basi ni kusema kile kinachokuwa kizuri kimeniletea kifo? Hapana hata kidogo! Ni zambi ndiyo iliyoniletea kifo. Lakini kusudi zambi ionekane kuwa zambi kweli kweli, ilipitia kwa njia ya kile kinachokuwa kizuri kwa kusababisha kifo changu. Hivi kwa njia ya amri ile, zambi ilizidi kujikamilisha kuwa zambi kabisa. Tunajua kwamba Sheria inaelekea maisha ya kiroho, lakini mimi ni mutu wa kimwili, kwa maana nimeuzishwa kama vile mutumwa wa zambi. Hakika sijui kitu ninachofanya. Kwa maana kile ninachotaka kufanya, sikifanyi; lakini kile ninachochukia, ndicho ninachofanya. Ikiwa kile ninachofanya ndicho nisichotaka, maana yake ninakubali ya kuwa Sheria ni nzuri. Basi sasa si mimi ninayekifanya, lakini ni zambi inayokaa ndani yangu. Kwa maana ninajua kwamba hakuna kitu kizuri kinachokaa ndani yangu, ni kusema katika hali yangu ya kimwili. Ni hivi kwa sababu ninakuwa na utashi wa kufanya jambo jema, lakini sifikii kulifanya. Jambo jema ninalotaka kufanya, silifanyi, lakini jambo baya nisilotaka, ndilo ninalofanya. Basi kama ninafanya kile nisichotaka kufanya, si mimi ninayekifanya, lakini ni ile zambi inayokaa ndani yangu. Basi ninatambua kanuni hii: wakati ninapotaka kufanya jambo jema, mara moja ninavutwa kufanya jambo baya. Ndani ya roho yangu ninapendezwa na Sheria ya Mungu, lakini ndani ya mwili wangu ninaona sheria ingine ikipigana na mafikiri yangu. Nayo inanifanya mufungwa wa sheria ya zambi inayotumika ndani ya mwili wangu. Ole kwangu, mimi mutu wa taabu! Ni nani atakayeniokoa kutoka katika mwili huu unaokuwa wa kufa? Mungu ashukuriwe kwa ajili ya Bwana wetu Yesu Kristo! Basi hivi kwa upande mumoja ninatumikia sheria ya Mungu kwa akili yangu, lakini kwa upande mwingine ninatumikia sheria ya zambi kwa hali yangu ya kimwili. Basi sasa hakuna azabu kwa wale wanaoungana na Yesu Kristo. Maana sheria ya Roho anayepana uzima kwa kuungana na Yesu Kristo imetuweka kuwa huru kutoka sheria ya zambi na ya kifo. Mungu alitimiza mambo yale Sheria ya Musa iliyoshindwa kuyatimiza, kwa sababu ya ukosefu wa nguvu unaotokana na hali zaifu ya kimwili. Mungu alitoa hukumu juu ya zambi inayotawala mwili kwa kutuma mwana wake wa peke katika hali ya kimutu, mwenye hali zaifu ya zambi kwa ajili ya kuondoa zambi. Alifanya vile kusudi maagizo ya haki ya Sheria yapate kutimizwa ndani yetu sisi tunaoishi kufuatana na uongozi wa Roho wa Mungu, lakini si kufuatana na hali yetu ya kimwili. Kwa maana wale wanaoishi kwa kufuatana na hali ya kimwili, wanashugulika na mambo yanayotakiwa na mwili lakini wale wanaoishi kufuatana na uongozi wa Roho wa Mungu wanashugulika na mambo yanayotakiwa na Roho yule. Kushugulika na mambo yanayotakiwa na hali ya kimwili kunaleta kifo lakini kushugulika na mambo yanayotakiwa na Roho wa Mungu kunaleta uzima na amani. Kwa maana wale wanaoshugulika na hali ya kimwili ni waadui za Mungu; hawatii sheria ya Mungu wala hawawezi kuitii. Watu wanaotawaliwa na hali ya kimwili hawawezi kumupendeza Mungu. Lakini ninyi sasa hamutawaliwi na hali yenu zaifu ya kimwili, lakini munatawaliwa na Roho Mutakatifu, ikiwa Roho wa Mungu anakaa ndani yenu. Na mutu yeyote asiyekuwa na Roho wa Kristo ndani yake, yeye si mutu wa Kristo. Lakini kama Kristo anakaa ndani yenu, ijapokuwa mwili wenu unakufa kwa sababu ya zambi, Roho ndiye uzima wenu kwa maana munahesabiwa haki mbele ya Mungu. Na kama Roho wa Mungu aliyemufufua Yesu anakaa ndani yenu, basi huyo aliyemufufua Kristo ataupatia mwili wenu unaokuwa wa kufa uzima kwa njia ya Roho wake anayekaa ndani yenu. Basi wandugu, tuko na deni, lakini si la kutimiza mapaswa ya hali yetu ya kimwili hata tuishi kufuatana na hali ile. Kwa maana kama mukiishi kufuatana na hali ya kimwili, mutakufa. Lakini kama mukiua matendo mabaya ya mwili kwa uwezo wa Roho Mutakatifu, mutaishi. Wote wanaoishi chini ya uongozi wa Roho wa Mungu ni watoto wa Mungu. Kwa maana hamukupewa roho anayewafanya muishi katika utumwa na kuwatia tena woga, lakini mulipewa Roho anayewafanya mukubaliwe kuwa watoto wa Mungu. Na kwa uwezo wa Roho huyo, tunaweza kumwita Mungu “Baba.” Roho huyo mwenyewe anahakikisha ndani ya roho zetu kwamba sisi ni watoto wa Mungu. Na kama sisi ni watoto, basi tutakuwa na sehemu katika urizi ule Mungu aliowaahidi watu wake, na tutashiriki pamoja na Kristo katika urizi ule; kwa maana kama tukiteswa pamoja naye tutatukuzwa pamoja naye vilevile. Ninaona kwamba mateso ya wakati huu wa sasa hayawezi kupima kulinganishwa na utukufu ambao Mungu atakaoonyesha kwetu waziwazi. Viumbe vyote vinangojea kwa hamu sana wakati Mungu atakapowaonyesha watoto wake waziwazi. Kwa maana viumbe vyote vimewekwa chini ya utawala wa mambo ya ovyo, si kwa mapenzi yao, lakini kwa sababu ya yule aliyewatia katika hali hiyo. Lakini kungali tumaini hili: siku moja viumbe hivi vitawekwa huru toka katika utumwa wa uharibifu na kushiriki katika uhuru wenye utukufu wa watoto wa Mungu. Kwa maana tunajua kwamba mpaka sasa viumbe vyote vinaugua kwa uchungu kama mwanamuke anayesikia maumivu ya kuzaa. Na si viumbe hivi tu; hata sisi tuliokwisha kuwa na Roho wa Mungu kama sehemu ya kwanza ya zawadi Mungu atakazotoa, tunaugua vilevile ndani yetu, tukingojea kukubaliwa na Mungu kuwa watoto wake, maana yake kukombolewa kwa kimwili. Kwa maana tumeokolewa, lakini ni kwa tumaini. Mutu akiona kitu anachokitumainia, hilo si tumaini tena, kwa maana nani anayeweza kuendelea kutumainia kitu anachokiona? Lakini tukitumainia kitu tusichokiona, tunakingojea kwa uvumilivu. Na ni hivi vilevile Roho wa Mungu anatusaidia katika uzaifu wetu, kwa maana hatujui kuomba sawa inavyopaswa. Lakini Roho wa Mungu yeye mwenyewe anatuombea kwa Mungu kwa kuugua kusikoweza kuelezwa. Na Mungu anayeona yanayokuwa ndani ya mioyo yetu, anajua nia ya Roho Mutakatifu, kwa maana Roho anawaombea watu wa Mungu kufuatana na mapenzi ya Mungu. Tunajua kwamba katika mambo yote Mungu anatumika kwa kuwajalia wale wanaomupenda, ndio wale walioitwa naye kufuatana na kusudi lake. Kwa maana wale Mungu aliowachagua tangu zamani, ndio aliofanya mupango juu yao tangu zamani, apate kuwafananisha na Mwana wake, kusudi Mwana wake akuwe muzaliwa wa kwanza wa wandugu wengi. Na wale Mungu aliowachagua tangia zamani, aliwaita vilevile; nao aliowaita, akawahesabia haki, nao aliowahesabia haki, akawatukuzisha vilevile. Basi kufuatana na mambo hayo, tuseme nini zaidi? Mungu akiwa upande wetu, ni nani anayeweza kupingana nasi? Yeye hakumwacha Mwana wake wa pekee, lakini alimutoa kwa ajili yetu sisi wote. Namna gani atakosa kutupatia vilevile vitu vyote kwa njia ya mwana wake? Ni nani anayeweza kuwashitaki watu ambao Mungu alijichagulia? Hakuna hata mumoja! Mungu peke yake amewahesabia haki mbele yake. Ni nani anayeweza basi kuwahukumu? Hakuna hata mumoja! Maana Yesu Kristo ndiye aliyekufa, na zaidi ya hiyo, alifufuka, na sasa anakaa na mamlaka kwa kuume kwa Mungu, na yeye ndiye anayetuombea. Ni nani anayeweza kututenga na upendo wa Kristo? Ni taabu, au huzuni, au mateso, au njaa, au ukosefu wa nguo, au hatari, au kifo? Kama vile Maandiko Matakatifu yanavyosema: “Kwa sababu yako tunauawa kila siku. Tunahesabiwa kama kondoo wa kuchinjwa.” Lakini katika mambo haya yote tunapata ushindi kabisa kwa njia ya yule aliyetupenda. Kwa maana ninajua hakika kwamba hakuna kitu kinachoweza kututenga na upendo wa Mungu: wala kifo, wala uzima, wala wamalaika, wala watawala, wala mambo ya sasa, wala mambo yatakayokuja, wala wenye uwezo, wala nguvu za juu, wala nguvu za chini, wala kiumbe kingine chochote hakitaweza kututenga na upendo wa Mungu aliouonyesha kwetu kwa njia ya Kristo Yesu Bwana wetu. Ninasema ukweli kwa kuungana na Kristo. Na kwa uongozi wa Roho Mutakatifu zamiri yangu inanihakikishia kwamba sisemi uongo: mimi nina huzuni kubwa na uchungu usiokuwa na mwisho ndani ya moyo wangu. Ingekuwa heri nilaaniwe na kutengwa na Kristo kwa ajili ya wandugu zangu wa damu, ndilo taifa la Waisraeli. Wao walikubaliwa na Mungu kuwa watoto wake, yeye aliwaonyesha utukufu, alifanya maagano nao, aliwapa Sheria, aliwaonyesha namna ya kumwabudu na kuwatolea ahadi zake. Wao ni wazao wa babu zetu, na Kristo alizaliwa kimwili katika kizazi chao. Yeye ndiye mukubwa kupita wote na Mungu anayesifiwa kwa milele! Amina. Sisemi kwamba ahadi ya Mungu haikutimia. Kwa maana si wote wanaotoka katika uzao wa Israeli ndio Waisraeli wa kweli, wala si wote wanaotoka katika uzao wa Abrahamu, ndio watoto wa kweli wa Abrahamu. Kwa kuwa Mungu alimwahidia Abrahamu: “Ni kwa njia ya Isaka utapata wazao watakaoitwa wako.” Maana yake, si wale waliozaliwa sawa na kawaida wanaohesabiwa kuwa watoto wa Mungu; lakini ni wale waliozaliwa kufuatana na ahadi ya Mungu ndio wanaohesabiwa kuwa wazao wake wa kweli. Kwa sababu hii ndiyo ahadi ya Mungu: “Kwa wakati kama huu, nitakuja tena, na Sara atazaa mutoto mwanaume.” Na si vile tu; Rebeka alikuwa na watoto wawili aliowazaa na mume mumoja, ndiye babu yetu Isaka. Kama vile Maandiko Matakatifu yanavyosema: “Nimemupenda Yakobo, lakini nimemuchukia Esau.” Basi tuseme nini? Mungu hafuati haki? Hapana hata kidogo! Kwa maana anamwambia Musa: “Nitamuhurumia yule ninayependa kumuhurumia; nitamurehemu yule ninayependa kumurehemu.” Basi mambo hayo, hayatokani na mapenzi ya mutu wala juhudi yake, lakini yanatokana na rehema ya Mungu. Mungu anamwambia mufalme wa Misri katika Maandiko Matakatifu: “Nimekusimika kuwa mufalme kwa sababu hii moja, ni kusudi kwa njia yako nipate kuonyesha uwezo wangu na kusudi jina langu lipate kutangazwa katika dunia yote.” Basi ni kusema kwamba Mungu anamuhurumia yule anayetaka, na kumufanya mugumu yule anayetaka. Labda utaniambia: “Ikiwa ni vile, sababu gani Mungu anawashitaki watu? Kwa maana hakuna anayeweza kupingana na mapenzi yake.” Halafu sasa wewe mwanadamu ni nani hata ubishane na Mungu? Chombo cha udongo hakiwezi kumwuliza mufinyanzi: “Kwa nini umenitengeneza hivi?” Mufinyanzi anaweza kufanya sawa vile anavyotaka na udongo. Toka donge moja la udongo anaweza kutengeneza chombo kimoja cha heshima na kingine cha matumizi ya kawaida. Basi kuna nini? Mungu alitaka kuonyesha kasirani yake na kutambulisha uwezo wake. Lakini aliwavumilia sana wale waliostahili kupatwa na kasirani yake na waliokuwa wametayarishwa kwa kuangamizwa. Vilevile alitaka kuonyesha uwingi wa utukufu wake kwa wale aliowasikilia huruma; wale ambao alitayarisha tangu zamani kwa kuwatukuzisha. Ndio sisi tulioitwa naye, si toka kati ya Wayuda tu, lakini toka kati ya watu wa mataifa mengine vilevile. Ni vile anavyosema katika maandiko haya ya nabii Hosea: “Wale waliokuwa si watu wangu nitawaita sasa ‘Watu wangu.’ Taifa lile nililokosa kulipenda nitaliita sasa ‘Mupendwa wangu.’ Na pahali pale walipoambiwa: ‘Ninyi si watu wangu!’ pale wataitwa ‘Watoto wa Mungu Mwenye Uzima.’ ” Isaya alisema kwa sauti juu ya Waisraeli: “Ijapokuwa Waisraeli ni wengi kama muchanga wa bahari, ni wachache tu watakaookolewa. Kwa maana Baba atatimiza kabisa kusudi lake juu ya dunia bila kukawia.” Ni kama vile Isaya alivyokuwa ametangulia kusema: “Kama Bwana wa Majeshi hangetuponyeshea wamoja wa wazao wetu, ingetutokea sawa Sodoma, ingegeuka kwetu sawa Gomora.” Basi tuseme nini? Watu wa mataifa mengine waliokosa kutafuta kuhesabiwa haki mbele ya Mungu wamehesabiwa haki mbele yake kwa njia ya imani. Na kwa ngambo ingine, Waisraeli waliokuwa wakitafuta Sheria kusudi kwa njia yake wapate kuhesabiwa haki mbele ya Mungu, hawakuifikia. Kwa sababu gani? Kwa sababu walitafuta haki ile, si kwa njia ya imani, lakini kwa njia ya matendo. Walijikwaa juu ya “lile jiwe la kukwalisha,” kama ilivyoandikwa katika Maandiko Matakatifu: “Angalia, ninaweka jiwe la kukwalisha katika Sayuni nalo ni la kuangusha. Lakini yule anayemwamini hatapata haya.” Wandugu zangu, kitu ninachotamani kwa moyo wote nami ninachomwomba Mungu kwa ajili ya Waisraeli, ni kwamba waokolewe. Kwa maana ninashuhudia kwamba wanajitoa kwa bidii kutumikia Mungu, lakini bidii ile haitokani na ufahamu wa kweli. Hawakufahamu namna Mungu anavyowahesabia watu haki na wakatafuta kusimamisha haki yao wenyewe. Wakakataa kufuata njia ya kuhesabiwa haki mbele ya Mungu. Kwa maana kwa njia ya Kristo, Sheria imepata kufikia ukomo wake kusudi kila mutu anayeamini apate kuhesabiwa haki mbele ya Mungu. Haya ndiyo mambo Musa aliyoandika juu ya kuhesabiwa haki mbele ya Mungu kwa njia ya kushika Sheria: “Mutu anayetimiza maagizo ya Sheria, ataishi kwa njia yake.” Lakini hivi ndivyo inavyosemwa juu ya kuhesabiwa haki kwa njia ya imani: “Usijiulize: ‘Ni nani atakayepanda mbinguni?’ ” (maana yake ni kumushusha Kristo toka kule.) Wala usijiulize: “Ni nani atakayeshuka katika kuzimu?” (maana yake kumupandisha Kristo toka kule kwenye wafu). Lakini inasemwa namna gani? “Neno la Mungu liko karibu nawe, liko ndani ya kinywa chako na ndani ya moyo wako.” Neno hili ni ujumbe tunaouhubiri juu ya imani. Kama ukiitikia kwa kinywa chako mwenyewe kwamba Yesu ni Bwana na kuamini katika moyo wako kwamba Mungu alimufufua, utaokolewa. Kwa maana mutu akiamini kwa moyo wake, Mungu anamuhesabia haki mbele yake; naye anapoitikia kwa kinywa chake, anaokolewa. Kwa maana Maandiko Matakatifu yanasema: “Kila mutu anayemwamini hatapata haya.” Basi hakuna tofauti kati ya Wayuda na watu wa mataifa mengine, kwa maana Bwana wa wote ni mumoja tu, na anawabariki sana wote wanaomusihi. Ni kama vile Maandiko Matakatifu yanavyosema: “Kila mutu anayemusihi Bwana, ataokolewa.” Basi namna gani watamusihi yule wasiyemwamini? Na namna gani watamwamini yule wasiyesikia habari zake? Na namna gani watasikia habari zake ikiwa hakuna wanaohubiri? Na namna gani watahubiri ikiwa hawatumwi? Ni kama inavyoandikwa katika Maandiko Matakatifu: “Angalia jinsi kunavyofurahisha kuja kwa wale wanaoleta habari njema.” Lakini wote hawakukubali ile Habari Njema. Kwa maana Isaya, alisema: “Ee Bwana, ni nani aliyeamini habari tulizotangaza?” Hivi basi imani inatokana na kusikia habari, na habari ile inatokana na neno la Kristo. Basi ninauliza: hawakusikia habari hii? Ndiyo, wameisikia! Kwa maana Maandiko Matakatifu yanasema: “Sauti yao imesikilika katika dunia yote, maneno yao yamefika pande zote za dunia.” Ninauliza tena: Waisraeli hawakufahamu kitu? Kwanza Musa alikuwa amekwisha kujibu: “Nitawafanya kuwa na wivu juu ya watu wasiokuwa taifa. Nitawakasirikisha ninyi kwa njia ya taifa pumbafu.” Isaya kwa uhodari anaongeza kusema maneno haya: “Nimepatikana kwa watu wasionitafuta, nimejifunua kwa watu wasioniuliza.” Lakini juu ya Waisraeli anasema hivi: “Muchana kutwa ninanyoosha mikono yangu kwa kuita taifa lenye uasi na ubishi.” Basi ninauliza: Mungu amewatupilia watu wake? Hapana hata kidogo! Maana kwa ngambo yangu, mimi ni Mwisraeli wa uzao wa Abrahamu, toka kabila la Benjamina. Mungu hakuwakataa watu wake aliojichagulia tangu mbele. Munakumbuka Maandiko Matakatifu yanayosema juu ya mashitaki ya Elia mbele ya Mungu juu ya Waisraeli? Yeye alisema: “Bwana, wamewaua manabii wako na kubomoa mazabahu zako; nami nimebaki peke yangu, nao wanatafuta kuniua.” Lakini Mungu alimujibu namna gani? Alimwambia: “Nimejiwekea watu elfu saba waliokataa kupiga magoti mbele ya mungu Bali.” Ni hivi vilevile kwa wakati huu wa sasa kunabaki wamoja ambao Mungu alichagua kwa neema yake. Na ikiwa walichaguliwa kwa neema ya Mungu, si kufuatana na matendo. Ingekuwa vile, neema isingekuwa neema tena. Nini basi? Taifa la Waisraeli halikupata kile walichokitafuta. Ni wachache tu ambao Mungu aliwachagua ndio waliokipata. Lakini wengine waliobaki, walifanywa kuwa wagumu, kama vile ilivyoandikwa katika Maandiko Matakatifu: “Mungu ameifanya mioyo yao kuwa migumu, macho yao yasipate kuona na masikio yao yasipate kusikia, na ni hivi wanavyokuwa hata leo.” Daudi anasema vilevile: “Karamu ziwageukie kama mitego ya kuwanasa, waanguke na kuazibiwa. Macho yao yatiwe giza wasione, na migongo yao ikunjame siku zote.” Basi ninauliza: Waisraeli wamejikwaa hata wakaanguka kabisa? Hapana hata kidogo! Lakini kutokana na kosa la Waisraeli, watu wa mataifa mengine wamepata kuokolewa, kusudi wayasikilie wivu. Kosa lao limeiletea dunia baraka nyingi, na upungufu wao umeleta baraka nyingi kwa watu wa mataifa mengi. Basi haitaleta baraka zaidi sana wakati Waisraeli wote watakapookoka? Sasa ninasema na ninyi watu wa mataifa mengine. Nami ninafurahia kazi yangu, kwa kuona nimetumwa kuwa muhubiri wa watu wa mataifa. Kwa sababu hii ninaweza kuwafanya watu wa taifa langu wawasikilie wivu, hata nipate kuwaokoa wamoja kati yao. Kwa maana ikiwa kukataliwa kwao na Mungu kumeleta upatanisho kati yake na dunia, basi si hakika kwamba kukubaliwa kwao na Mungu kutaleta uzima kwa wale waliokufa. Donge la kwanza la unga wenye kupondwa likitolewa kwa Mungu, mikate itakuwa yake vilevile. Na kama shina la muti likitolewa kwa Mungu, matawi yatakuwa yake vilevile. Matawi mamoja ya muzeituni uliopandwa yamekatwa, na chipukizi la muzeituni uliojiotesha katika pori umepandikizwa kwenye nafasi yao. Na sasa unafaidia vilevile utomvu unaotoka ndani ya shina la yule muzeituni uliopandwa. Basi musizarau yale matawi yaliyokatwa. Ninyi hamuna cha kujivunia, kwa maana si ninyi munaoshikilia shina, lakini ni shina linalowashikilia. Labda utaweza kuniambia: “Matawi yale yalikatwa kusudi mimi nipandikizwe kwenye nafasi yao.” Unasema ukweli. Yamekatwa kwa sababu yalikataa kuamini na wewe unasimama imara katika imani yako. Sasa usijivune, lakini uogope! Kwa maana ikiwa Mungu hakuachilia yale matawi ya asili kuendelea kukomaa, namna gani atakuachilia wewe? Basi ufikiri juu ya wema wa Mungu na ukali wake vilevile. Yeye ni mukali kwa wale walioanguka, lakini yeye ni mwema kwako, ikiwa utaendelea katika wema wake. Kama si vile, wewe vilevile utakatwa. Na kama Wayuda wasipoendelea kukataa kuamini, watapandikizwa kwenye nafasi ile walipokuwa mbele, kwa maana Mungu yuko na uwezo wa kuwapandikiza tena. Ninyi watu wa mataifa mengine ni kama tawi la muzeituni wa pori lililokatwa na kisha likapandikizwa ndani ya muzeituni uliopandwa, umbalimbali na kawaida. Wayuda ni kama muzeituni huu uliopandwa; na si neno gumu basi kwa Mungu kupandikiza tena matawi yaliyokatwa katika muti wao wenyewe. Wandugu zangu, sitaki mukose kujua siri hii, kusudi musijione kuwa wenye akili sana. Siri ile ni hii: Waisraeli wamoja wataendelea kuwa wagumu mpaka watu wa mataifa mengine kwa jumla watakapokuja kwa Mungu. Na halafu taifa lote la Israeli litaokolewa kama vile inavyoandikwa katika Maandiko Matakatifu: “Mukombozi atatokea Sayuni, atakomesha uovu kati ya wazao wa Yakobo. Na hili ndilo agano nitakalofanya nao, wakati nitakapowasamehe zambi zao.” Wayuda wamegeuka waadui za Mungu kwa sababu ya kukataa Habari Njema, na jambo hilo limekuwa faida kwenu ninyi watu wa mataifa mengine. Lakini wao ni wapendwa wake kufuatana na vile wamechaguliwa naye, kwa njia ya babu zao. Kwa maana Mungu habadilishi mafikiri juu ya zawadi anazotoa, wala juu ya wale anaowachagua. Zamani ninyi mulimwasi Mungu, lakini sasa amewahurumia kutokana na uasi wa Wayuda. Ni hivi vilevile, kutokana na vile mulivyohurumiwa, sasa wao wanamwasi Mungu, kusudi wao vilevile wapate kuhurumiwa na Mungu. Maana Mungu amewafanya watu wote kama wafungwa kwa sababu ya kuasi kwao, kusudi awahurumie wote. Utajiri wa Mungu, hekima na ufahamu wake ni vikubwa kupita kipimo! Hakuna anayeweza kuvumbua kusudi lake wala kuelewa mipango yake! Kama vile Maandiko Matakatifu yanavyosema: “Ni nani anayejua mafikiri ya Bwana? Ni nani anayeweza kuwa mushauri wake? Ni nani anayeweza kumupa Mungu kitu kwanza, kusudi naye apate kumurudishia?” Kwa maana vitu vyote vinatoka kwake, navyo viko kwa uwezo wake na kwa ajili yake. Atukuzwe hata milele! Amina. Basi wandugu zangu, kufuatana na vile Mungu alivyoonyesha huruma yake kwetu, ninawasihi mujitoe wenyewe kwake kuwa sadaka yenye uzima, takatifu na yenye kumupendeza. Hii ndiyo njia ya kweli ya kumwabudu. Musifuate mwenendo wa siku hizi, lakini muache Mungu awabadilishe kwa kugeuza upya nia zenu, hata mukuwe na mawazo mapya. Kwa hiyo mutaweza kutambua mapenzi ya Mungu. Mutajua mambo gani yanayokuwa mema, yanayomupendeza Mungu na yanayokuwa makamilifu. Kufuatana na neema niliyopewa na Mungu, ninawaambia ninyi wote: mutu asijiwazie kuwa na ukubwa kupita vile inavyomustahili. Lakini mukuwe na mawazo ya ukadirifu, kila mumoja kulingana na kipimo cha imani aliyopewa na Mungu. Katika mwili mumoja kuna viungo vingi, lakini viungo hivi vyote havina kazi moja. Hivi vilevile, sisi tunaokuwa wengi tumekuwa mwili mumoja katika kuungana kwetu na Kristo, na sisi wote ni viungo kila mumoja kwa mwingine. Tuko na zawadi mbalimbali kwa kadiri ya neema tuliyopewa na Mungu. Aliyepewa zawadi ya unabii, anapaswa kutabiri kwa kadiri ya imani yake. Aliyepewa zawadi ya utumishi, atumike. Aliyepewa zawadi ya kufundisha, afundishe. Aliyepewa zawadi ya kuonya wengine, awaonye. Aliyepewa zawadi ya kutoa, atoe kwa moyo mweupe. Anayesimamia wengine, awasimamie kwa bidii. Aliyepewa zawadi ya kuhurumia wengine, afanye vile kwa furaha. Upendo wenu ukuwe pasipo udanganyifu. Muchukie chochote kinachokuwa kibaya, mushikamane na kinachokuwa chema. Mupendane ninyi kwa ninyi kwa kweli kama vile wandugu, nanyi muheshimiane ninyi kwa ninyi. Musikuwe wavivu katika kazi lakini mukuwe na bidii, mukimutumikia Bwana kwa juhudi. Mufurahi mukiwa na tumaini, muvumilie katika mateso, mudumu katika kuomba. Muwasaidie watu wa Mungu katika mahitaji yao na muwakaribishe wageni. Mumwombe Mungu awabariki wale wanaowatesa; muwaombee baraka wala musiwalaani. Mufurahi pamoja na wenye kufurahi. Mulie pamoja na wenye kulia. Mukuwe na masikilizano kati yenu. Musikuwe na nia ya kujitukuza, lakini mukubali kuishi katika unyenyekevu. Musijiwazie kuwa wenye akili sana. Musimurudishie mutu ubaya kwa ubaya. Mukuwe na roho ya kufanya mema mbele ya watu wote. Kama ikiwezekana, kwa upande wenu, muishi katika amani na watu wote. Wandugu wapendwa, musilipize kisasi ninyi kwa ninyi, lakini mumwachie Mungu wakati wa kutenda kufuatana na kasirani, maana imeandikwa katika Maandiko Matakatifu: “Ni kazi yangu kulipiza kisasi. Ni mimi nitakayelipiza.” Lakini kama vile Maandiko Matakatifu yanavyosema: “Adui yako akisikia njaa, umupe chakula; kama akisikia kiu, umupe kinywaji. Maana kwa kufanya hivi utamupatisha haya kama vile ungemubebesha makaa ya moto juu ya kichwa.” Usijiachilie kushindwa na ubaya, lakini ushinde ubaya kwa kutenda mema. Kila mutu anapaswa kutii wakubwa wenye mamlaka. Maana hakuna mamlaka isiyotoka kwa Mungu; nao wakubwa wanaotawala wamesimikwa na Mungu. Kwa hiyo yeye anayepingana na mwenye mamlaka anapinga amri ya Mungu, nao wanaofanya vile wanajiletea azabu wenyewe. Kwa maana wanaofanya mema hawaogopi watawala, lakini wale wanaofanya mabaya. Unataka kuishi bila kumwogopa mwenye mamlaka? Basi fanya mema naye atakusifu, maana yeye anamutumikia Mungu kwa faida yako. Lakini kama ukifanya mabaya, umwogope kwa sababu yeye yuko na uwezo kwa kuazibu. Yeye anamutumikia Mungu wa kuazibu wale wanaofanya mabaya. Kwa sababu hii ni lazima kuwatii wenye mamlaka, si kwa sababu ya kuogopa azabu ya Mungu tu, lakini tena kwa sababu ya kusongwa na zamiri. Kwa sababu hii vilevile munalipa kodi, maana watawala wanamutumikia Mungu wakijitoa kwa kazi ile. Mumupe kila mutu haki yake: mulipishaji wa kodi, mumulipe kodi; mulipishaji wa ushuru, mumulipe ushuru. Mumuheshimu anayestahili kuheshimiwa na mumutukuze anayestahili kutukuzwa. Musikuwe na deni la mutu yeyote. Deni moja munalopaswa kuwa nalo ni kupendana. Kwa maana yule anayemupenda mwenzake ametimiza Sheria kabisa. Kwa hiyo amri hizi: “Usizini, usiue, usiibe, usitamani,” pamoja na zingine zote, zinafungwa katika amri hii moja: “Umupende mwenzako sawa vile unavyojipenda mwenyewe.” Anayemupenda mwenzake hawezi kumutendea vibaya. Basi Sheria inatimizwa kwa njia ya upendo. Mufanye vile, maana munajua tunaishi katika siku gani sasa. Saa ya kuamuka katika usingizi wenu imetimia, kwa maana sasa wakati wetu wa kuokolewa unakaribia kuliko vile ilivyokuwa wakati tulipoanza kuamini. Usiku umepita, na muchana unakaribia. Basi tutupilie mbali matendo ya giza na kuvaa silaha za kupigana nazo wakati wa mwangaza. Tukuwe na mwenendo muzuri unaostahili wakati wa muchana, tukijilinda na ulafi na ulevi, uasherati na uzinzi, magombano na wivu. Lakini Bwana Yesu akuwe kama vile silaha munayobeba, musijiachilie kuvutwa na hali yenu ya kimwili hata mutimize tamaa zake. Mumupokee yule anayekuwa zaifu katika imani pasipo kubishana naye juu ya mawazo yake. Kwa mufano, mutu mumoja kutokana na imani yake anaona kwamba anaweza kula kila chakula, lakini mwingine kutokana na imani yake zaifu, anakula tu mboga za majani. Yule anayekula kila chakula asimuzarau yule asiyekula kila chakula. Vilevile yule asiyekula kila chakula asimuhukumu yule anayekikula, kwa maana Mungu amemupokea. Wewe ni nani unayehukumu mutumishi wa mwingine? Akisimama imara katika kazi yake au akianguka, hilo ni shauri la bwana wake. Naye atasimama imara maana Bwana yuko na uwezo wa kumusimamisha. Watu wamoja wanahesabu siku fulani kuwa yenye maana zaidi kuliko siku zingine, lakini wengine wanahesabu siku zote kuwa sawasawa. Kwa hiyo kila mutu asadiki sawa vile anavyowaza yeye mwenyewe. Mutu yeyote anayeshugulika juu ya siku fulani, anafanya hivi kwa kumutukuza Bwana. Yule anayekula kila chakula, anafanya vile kwa kumutukuza Bwana; maana anamushukuru Mungu kwa ajili ya chakula chake. Na asiyekula kila chakula anafanya hivi vilevile kwa kumutukuza Bwana na kumushukuru Mungu. Kwa maana hakuna hata mutu mumoja kati yetu anayeishi kwa ajili yake mwenyewe, wala hakuna anayekufa kwa ajili yake mwenyewe. Maana kama tunaishi, tunaishi kwa ajili ya Bwana, na kama tunakufa, tunakufa kwa ajili ya Bwana. Basi ikiwa tunaishi, au ikiwa tunakufa, sisi ni watu wa Bwana. Ni kwa sababu hii Kristo alikufa na kufufuka kusudi apate kuwa Bwana wa waliokufa na wa wanaokuwa wazima vilevile. Lakini wewe, kwa sababu gani unamuhukumu ndugu yako? Au wewe kwa sababu gani unamuzarau ndugu yako? Maana sisi wote tutasimama kwa kusambishwa mbele ya tribinali ya Mungu. Kwa maana imeandikwa katika Maandiko Matakatifu: “Bwana anasema: Kama vile ninavyoishi, kila mutu atapiga magoti mbele yangu, na kila mutu ataitikia kwamba mimi ni Mungu.” Kwa hiyo kila mumoja kati yetu atajitetea mwenyewe kwa Mungu. Basi tusihukumiane tena sisi wenyewe. Lakini tafazali mukamate kusudi hili: mutu asifanye kitu kinachoweza kumukwaza au kumwangusha ndugu yake katika zambi. Kufuatana na vile ninaungana na Bwana Yesu, ninajua hakika kwamba hakuna kitu kinachohesabiwa kichafu katika hali yake ya asili. Lakini kama mutu akihesabu kwamba kitu fulani ni kichafu, basi kitu kile ni kichafu kwake. Kama ukimuhuzunisha ndugu yako kwa sababu ya chakula unachokula, wewe hautendi tena kufuatana na upendo. Kwa njia ya chakula chako usimupoteze mutu ambaye Kristo alikufa kwa ajili yake. Basi musikubali kitu kile kinachoonekana kwenu kuwa kizuri kizarauliwe. Kwa maana kazi ya Ufalme wa Mungu si kushugulika na mambo ya kula na kunywa, lakini ni kushugulika na haki, amani na furaha vinavyotolewa na Roho Mutakatifu. Na yeyote anayemutumikia Kristo kwa njia hiyo anamupendeza Mungu, naye anapata kuwa mwenye kustahili mbele ya watu. Basi kwa hiyo tujikaze sana kufanya mambo yale yanayoleta amani na yanayotusaidia kujengana katika imani. Usiharibu kazi ya Mungu kwa sababu ya maneno ya chakula. Hakika vyakula vyote vinaruhusiwa kukuliwa, lakini ni vibaya kwa mutu kula chakula kinachoweza kukwaza mwingine. Ni vema kuacha kula nyama, kunywa divai na kujizuiza kufanya chochote kinachoweza kumukwaza ndugu yako. Ulinde kwa ajili yako mwenyewe kile unachoaminia juu ya mambo yale mbele ya Mungu. Heri mutu asiyejihukumu katika kusudi lake. Lakini mutu anayekuwa na mashaka juu ya chakula anachokula, Mungu anamuhukumu, kwa sababu hatendi kufuatana na imani. Na kitendo chochote kisichotokana na imani ni zambi. Sisi tunaokuwa na nguvu katika imani tunapaswa kubeba muzigo wa uzaifu wa wale wasiokuwa na nguvu. Tusifanye tu mambo yanayotupendeza wenyewe. Lakini kila mumoja wetu anapaswa kumupendeza mwingine kwa kumutendea mema na kuweza hivi kumujenga katika imani. Kwa maana hata Kristo hakufanya mambo yanayomupendeza mwenyewe sawa vile ilivyoandikwa katika Maandiko Matakatifu: “Matusi wanayokutukana, yananiangukia.” Na yote yaliyoandikwa zamani katika Maandiko Matakatifu yameandikwa kwa ajili ya kutufundisha sisi, kusudi tuendelee kuchunga tumaini kwa njia ya kuvumilia na kufarijiwa sawa tunavyofundishwa katika Maandiko Matakatifu. Basi, Mungu anayewapa watu nguvu ya kuvumilia na kufarijika awape kuwa na nia moja mukifuata mufano wa Kristo Yesu. Hivi kusudi mutaweza kwa nia moja na kwa sauti moja kumutukuza Mungu, Baba wa Bwana wetu Yesu Kristo. Basi mupokeane kwa upendo sawa vile Kristo alivyotupokea kusudi Mungu apate kutukuzwa. Kwa maana ninawaambia wazi kwamba Kristo alifanya utumishi kwa ajili ya Wayuda kwa kuhakikisha kuwa Mungu ni mwaminifu na kusudi atimize ahadi zile babu zetu walizopewa. Vilevile ilikuwa kusudi watu wa mataifa mengine wamutukuze Mungu kwa huruma yake, kama inavyoandikwa katika Maandiko Matakatifu: “Kwa hiyo nitakutukuza kati ya mataifa, nitakuimbia sifa.” Na tena Maandiko yanasema: “Ninyi watu wa mataifa yote mufurahi pamoja na taifa lake!” Na tena hivi: “Enyi mataifa yote, mumusifu Bwana; enyi watu wote, mumusifu!” Isaya naye anasema: “Muzao wa Yese atatokea, atatawala watu wa mataifa, nao watamutumainia.” Basi, Mungu anayekuwa musingi wa matumaini, awajaze furaha kamili na amani kutokana na imani yenu; hata tumaini lenu lipate kuongezeka kwa nguvu ya Roho Mutakatifu. Wandugu zangu, kwa ngambo yangu ninajua hakika kwamba ninyi munajaa wema, nanyi munafahamu yote yanayofaa na munaweza kushauriana vizuri. Lakini mara moja moja nimewaandikia kwa uhodari juu ya mambo fulani kusudi niwakumbushe tena mambo yale. Nimefanya vile kutokana na neema ile niliyopewa na Mungu kuwa mutumishi wa Yesu Kristo kwa watu wa mataifa mengine. Ninafanya kazi ya ukuhani ya kuhubiri Habari Njema ya Mungu, kusudi watu wa mataifa mengine wapate kuwa kama sadaka inayokubaliwa na Mungu na iliyotakaswa na Roho Mutakatifu. Basi katika kuungana kwangu na Kristo, ninaweza kujisifu kwa ajili ya kazi hii ninayomutumikia Mungu. Kwa maana sitasubutu kuongeza kitu kingine, isipokuwa tu kile Kristo alichotimiza kwa njia yangu kusudi watu wa mataifa wapate kumutii Mungu. Alifanya vile kwa njia ya yale aliyoniwezesha kusema na kutenda, kwa njia ya uwezo wa vitambulisho na maajabu, na kwa uwezo wa Roho Mutakatifu. Hivi tokea Yerusalema mpaka kufika katika jimbo la Iliriko nimehubiri fasi zote Habari Njema ya Kristo. Nayo nia moja niliyokuwa nayo ni kuhubiri tu Habari Njema fasi zote ambapo habari za Kristo zilipokuwa hazijasikilika bado. Nilikusudia vile kusudi nisijenge juu ya musingi uliowekwa na mutu mwingine, kama vile inavyoandikwa katika Maandiko Matakatifu: “Wale ambao hawajaambiwa bado habari zake, watamwona. Wale hawajazielezwa bado, watazifahamu.” Hiyo ndiyo sababu iliyonizuiza mara nyingi kufika kule kwenu. Lakini kwa sasa nimemaliza kazi yangu katika pande hizi za inchi, na tena tangu miaka mingi nina hamu sana ya kuja kuwaona; kwa hiyo nitawafikia nitakapokwenda Spania. Ninatumaini kupitia kule na kuonana nanyi, na kisha kufurahi kwanza pamoja nanyi kwa muda mufupi, ningetamani kupata musaada wenu kwa ajili ya safari ile. Lakini sasa ninakwenda kwanza Yerusalema kuwasaidia watu wa Mungu kule. Kwa maana imependeza makanisa ya Makedonia na ya Akaya kukusanya mali kwa kuwasaidia wamasikini wanaokuwa kati ya watu wa Mungu kule Yerusalema. Ndiyo wamefanya vile kwa mapenzi yao, lakini vilevile ilikuwa mapaswa kwao kuwasaidia. Kwa maana ikiwa watu wa mataifa wameshirikiana baraka za kiroho na Wayuda, imewapasa watu wa mataifa mengine kuwasaidia Wayuda katika mahitaji ya kimwili. Basi nitakapomaliza kazi ile na kuwafikishia mali iliyokusanywa, nitapitia kwenu, nikiwa katika safari yangu ya kwenda Spania. Nami ninajua kwamba wakati nitakapokuja kwenu, nitakuja na baraka nyingi sana kutoka kwa Kristo. Wandugu zangu, ninawasihi kwa ajili ya Bwana wetu Yesu Kristo na kwa ajili ya upendo unaoletwa na Roho wa Mungu, muungane nami kwa kuniombea kwa Mungu. Muniombee kusudi nisipate hasara toka kwa watu wale wasioamini wanaokuwa Yudea na kusudi musaada ninaoupeleka Yerusalema upate kupokelewa vizuri kule na watu wa Mungu. Na hivi Mungu akitaka, nitakuja kwenu kwa furaha, nami nitapata kutulizwa moyo kati yenu. Basi Mungu anayeleta amani akuwe pamoja nanyi wote. Amina! Ninawatumia dada yetu mwamini Foibe, anayekuwa musaidizi wa kanisa la Kenkurea. Mumupokee kwa ajili ya Bwana, kama vile watu wa Mungu wanavyopaswa kufanya. Mumusaidie katika kila jambo atakalohitaji toka kwenu, maana yeye amewasaidia watu wengi na hata mimi peke yangu vilevile. Munisalimie Prisila na Akila, watumishi wenzangu katika kazi ya Yesu Kristo. Wao walijitolea kufa kwa kuokoa maisha yangu. Ninawashukuru, wala si mimi peke yangu tu, nayo makanisa yote ya inchi za watu wa mataifa wanawashukuru vilevile. Munisalimie vilevile kanisa linalokusanyika katika nyumba yao. Munisalimie mupendwa wangu Epeneto, anayekuwa mwamini wa kwanza wa Kristo katika jimbo la Azia. Munisalimie Maria, aliyewashugulikia sana. Munisalimie wanainchi wenzangu Androniko na Yunia, waliofungwa pamoja nami katika kifungo. Wao wanasifiwa sana kati ya mitume, nao walikuwa katika Kristo mbele yangu. Munisalimie Ampuliato, mupendwa wangu katika Bwana. Munisalimie Urbano, mutumishi mwenzetu katika kazi ya Kristo, na Staki, mupendwa wangu. Munisalimie Apele, aliyehakikisha uaminifu wake katika Kristo. Munisalimie watu wanaoishi katika nyumba ya Aristobulo. Munisalimie Herodio, mwanainchi mwenzangu. Munisalimie watu wanaoishi katika nyumba ya Narkiso, wanaomwamini Bwana. Munisalimie Tirifena na Tirifosa, wale wanawake wanaomushugulikia Bwana, na mupendwa wangu Persi, aliyemushugulikia sana Bwana. Munisalimie Rufo, mutumishi hodari katika kazi ya Bwana, na mama yake ninayemuhesabu kama mama yangu vilevile. Munisalimie Asinkristo, Fulego, Herme, Patroba, Herma, na wandugu wanaoshiriki pamoja nao. Munisalimie Filologo na Yulia, Nereo na dada yake, na Olimpa, na watu wote wa Mungu wanaoshiriki pamoja nao. Musalimiane kwa upendo wa kikristo. Makanisa yote ya Kristo yanawasalimia. Wandugu zangu, ninawasihi, mufanye angalisho na wale wanaoleta matengano na mambo ya kuwapotoa wengine wakipinga mafundisho muliyopokea. Mujitenge mbali nao. Kwa maana watu wa namna hii hawamutumikii Bwana wetu Kristo, lakini wanatumikia tu tumbo yao wenyewe. Tena kwa maneno yao matamu na ya kujipendekeza wanadanganya watu wasiokuwa na makosa. Watu wote wanajua namna munavyomutii Bwana, na kwa sababu hii ninafurahi kwa ajili yenu. Lakini ninataka mukuwe wenye hekima kwa kutenda mema, na mukuwe safi mukijitenga na mambo mabaya. Mungu, anayeleta amani, atamupondaponda sasa hivi Shetani chini ya miguu yenu. Neema ya Bwana wetu Yesu Kristo ikuwe pamoja nanyi. Timoteo, mutumishi mwenzangu anawasalimia, nao Lukio, Yasoni, na Sosipateri, wanainchi wenzangu wanawasalimia vilevile. Mimi Tertio, niliyeandika barua hii, ninawasalimia kwa jina la Bwana. Gayo, aliyenikaribisha na anayekaribisha kanisa zima kwa kukusanyika kwake, anawasalimia. Erasto, mulinzi wa mali ya muji, pamoja na ndugu yetu Kwarto, wanawasalimia. [ Tunawatakia ninyi wote neema kutoka kwa Bwana wetu Yesu Kristo. Amina.] Mungu asifiwe! Yeye yuko na uwezo wa kuwaimarisha katika imani juu ya Habari Njema ninayotangaza kwa kuhubiri ujumbe juu ya Yesu Kristo, kufuatana na ufunuo wa siri iliyofichwa tangia zamani za kale na kale. Lakini sasa yamefunuliwa na maandiko ya manabii kufuatana na amri ya Mungu wa milele, kusudi mataifa yote yapate kumwamini na kumutii. Basi Mungu anayekuwa peke yake mwenye hekima atukuzwe milele na milele kwa njia ya Yesu Kristo! Amina. Barua hii inatoka kwangu mimi Paulo na kwa ndugu yetu Sositeni. Ni mimi niliyeitwa na Mungu kwa mapenzi yake kuwa mutume wa Kristo Yesu. Tunawaandikia ninyi kanisa la Mungu linalokuwa Korinto, ninyi ambao mumetakaswa kwa njia ya kuungana kwenu na Yesu Kristo na mumeitwa na Mungu kuwa watu wake. Vilevile barua hii ni kwa wote wanaoabudu jina la Bwana Yesu Kristo fasi zote, anayekuwa Bwana wao na Bwana wetu vilevile. Tunawatakia neema na amani kutoka kwa Mungu Baba yetu na kwa Bwana Yesu Kristo. Ninamushukuru Mungu wangu siku zote kwa ajili yenu, kwa sababu ya neema Mungu aliyowapa ninyi kwa njia ya Yesu Kristo. Kwa maana katika kuungana kwenu na Kristo, mumejaliwa katika vitu vyote, zaidi sana katika mambo yanayoelekea masemi na ufahamu. Ile inatokana na vile ujumbe juu ya Kristo umehakikishwa kwa nguvu kati yenu, hata hamukosewi zawadi yoyote ya Mungu, mukiwa mukingojea wakati Bwana wetu Yesu Kristo atakapoonekana. Ni yeye atakayewasimamisha ninyi imara mpaka mwisho kusudi musishitakiwe juu ya kosa lolote Siku ile ya kurudi kwa Bwana wetu Yesu Kristo. Mungu ni mwaminifu katika ahadi zake, yeye aliyewaita ninyi muishi katika ushirika pamoja na Mwana wake Yesu Kristo, Bwana wetu. Wandugu zangu, ninawasihi ninyi kwa jina la Bwana wetu Yesu Kristo, mukuwe na masikilizano kusudi matengano yasikuwe katikati yenu. Muishi katika umoja kabisa mukiwa na nia moja na wazo moja. Kwa maana, wandugu zangu, nimepata habari zenu kwa njia ya jamaa ya Kloe kwamba kuko ugomvi katikati yenu. Ninataka kusema: kila mumoja kati yenu anasema maneno yake mbalimbali. Mumoja anasema: “Mimi ni wa Paulo,” mwingine anasema: “Mimi ni wa Apolo,” mwingine anasema: “Mimi ni wa Petro,” na mwingine anasema: “Mimi ni wa Kristo.” Munafikiri kwamba Kristo amegawanyika? Paulo ndiye aliyetundikwa juu ya musalaba kwa ajili yenu? Au mumebatizwa kwa jina la Paulo? Ninamushukuru Mungu kuwa sikubatiza hata mumoja wenu isipokuwa Krispo na Gayo. Hivi hakuna anayeweza kusema kwamba amebatizwa kwa jina langu. Ni kweli, nilibatiza vilevile jamaa ya Stefano, zaidi ya wale sikumbuki kama nilibatiza mutu mwingine. Kristo hakunituma kwa kubatiza, lakini amenituma kwa kutangaza Habari Njema. Amenituma kuitangaza bila kutumia hekima ya usemi, kusudi uwezo unaotokana na kufa kwa Kristo juu ya musalaba usihesabiwe kuwa bure. Hivi, mahubiri ya kufa kwa Kristo juu ya musalaba yanahesabiwa kuwa upumbafu kwa wale wanaopotea. Lakini kwa sisi tunaookolewa ni uwezo wa Mungu. Kwa maana Maandiko Matakatifu yanasema: “Nitaharibu hekima ya wenye hekima, Nitapoteza akili ya wenye akili.” Basi, tuseme nini juu ya wenye hekima, walimu wa Sheria, nao wafundi wa usemi siku hizi? Mungu ameonyesha wazi kwamba hekima ya dunia hii ni upumbafu! Mungu alikusudia kuwaokoa wale wanaomwamini kwa njia ya mahubiri tunayotangaza yanayoonekana kuwa mambo ya upumbafu. Amefanya vile kwa sababu, kwa njia ya hekima yao ya kimutu, watu hawakumutambua Mungu na hekima yake ya kimungu. Wayuda wanaomba kuonyeshwa vitambulisho nao Wagriki wanatafuta hekima. Lakini sisi tunamuhubiri Kristo aliyetundikwa juu ya musalaba, na mahubiri hayo yanahesabiwa kama kikwazo kwa Wayuda na upumbafu kwa watu wa mataifa mengine. Lakini kwa wale walioitwa na Mungu, ikiwa Wayuda au wasiokuwa Wayuda, Kristo ni kitambulisho cha uwezo na hekima ya Mungu. Kwa maana mambo wanayomuhesabilia Mungu kuwa ya upumbafu, yanapita hekima ya watu; nayo mambo yale wanayomuhesabilia kuwa ya uzaifu yanapita nguvu za watu. Basi wandugu zangu, mukumbuke vile mulivyoitwa na Mungu, kwamba si wengi kati yenu wenye hekima kufuatana na mafikiri ya watu; si wengi kati yenu wanaokuwa wenye nguvu, wala wenye vyeo. Lakini Mungu anachagua vitu ambavyo watu wanahesabu kuwa vya upumbafu kusudi apatishe wenye hekima haya, naye amechagua vitu wanavyohesabu kuwa vya uzaifu kusudi apatishe wenye nguvu haya. Mungu amechagua vitu ambavyo watu wanahesabu kuwa vya hali ya chini na vyenye kuzarauliwa, visivyokuwa na maana mbele ya macho ya watu, kusudi aharibu vile wanavyohesabu kuwa vya lazima. Alifanya vile kusudi hata mutu mumoja asijivune mbele yake. Lakini Mungu amewaunganisha na Yesu Kristo, naye amemufanya Kristo kuwa hekima yetu. Kwa njia ya Kristo tunahesabiwa haki mbele ya Mungu, tumekuwa watu watakatifu wa Mungu, na kukombolewa toka zambi zetu. Kama vile Maandiko Matakatifu yanavyosema: “Anayetaka kujivuna, ajivune kwa ajili ya Bwana.” Wandugu zangu, wakati nilipokuja kwenu kuwapasha habari ya siri ya Mungu, sikutumia maneno magumu wala hekima ya dunia. Kwa maana wakati nilipokuwa pamoja nanyi nilikusudia nisijue mambo mengine lakini Yesu Kristo tu na habari ya kufa kwake juu ya musalaba. Sababu ya hii nilikuwa kwenu katika hali ya uzaifu na woga, mwenye kutetemeka sana. Mafundisho yangu na mahubiri yangu hayakutolewa kwa maneno ya werevu na hekima ya kimutu, lakini katika onyesho la uwezo wa Roho wa Mungu, kusudi imani yenu isikuwe katika hekima ya watu, lakini katika uwezo wa Mungu. Ingawa vile, mimi ninatangaza mambo ya hekima kwa watu waliokomaa kiroho. Lakini mambo haya si ya hekima ya kidunia, wala ya watawala wa dunia hii watakaoangamizwa. Ninatangaza hekima ya siri ya Mungu, hekima iliyofichwa kwa watu, na iliyopangwa na Mungu mbele ya kuumbwa kwa dunia kwa ajili ya utukufu wetu. Hakuna hata mutawala mumoja kati ya watawala wa dunia hii aliyeelewa hekima ile. Kama wangeielewa wasingemutundika Bwana wa utukufu juu ya musalaba. Lakini ni kama vile Maandiko Matakatifu yanavyosema: “Mambo yale ambayo hakuna mutu aliyepata kuyaona wala kuyasikia, mambo yale ambayo hakuna mutu aliyepata kufikiri juu yake, ndiyo yale Mungu aliyowatayarishia wale wanaomupenda.” Lakini Mungu ametufunulia sisi siri yake kwa njia ya Roho wake. Maana Roho anachunguza vitu vyote, hata mipango ya Mungu inayofichwa kabisa. Hakuna mutu anayeweza kujua mawazo ya mutu mwingine isipokuwa tu roho ya mutu inayokuwa ndani yake. Vilevile, hakuna anayejua mawazo ya Mungu isipokuwa Roho wa Mungu tu. Na sisi hatukupokea roho ya dunia hii, lakini tulipokea Roho anayetoka kwa Mungu, kusudi tupate kujua vitu vyote tulivyojaliwa kwa neema ya Mungu. Nasi tunaposema hatutumii maneno yanayotokana na hekima ya kimutu, lakini maneno yanayotokana na Roho wa Mungu, tukieleza maneno ya kiroho kwa watu wanaokuwa wa Roho. Lakini mutu anayefuata hali yake ya kidunia hawezi kukubali maneno yanayotoka kwa Roho yule. Kwa sababu anayaona kuwa ni upumbafu kwake, naye hawezi kuyaelewa kwa maana yanatambulikana tu kwa njia ya Roho. Mutu anayekuwa na Roho wa Mungu anahukumu mambo yote, lakini hakuna mutu anayeweza kumuhukumu. Kama vile Maandiko Matakatifu yanavyosema: “Ni nani anayejua mawazo ya Bwana? Ni nani anayeweza kumushauria?” Lakini sisi tuko na mawazo yanayotoka kwa Kristo. Kweli wandugu zangu, sikuweza kusema nanyi kama watu wanaotawaliwa na Roho wa Mungu, lakini kama watu wanaotawaliwa na mambo ya kidunia. Mungali kama watoto wachanga katika mambo ya Kikristo. Niliwakunywesha maziwa, sikuwapa chakula kigumu, kwa maana mulikuwa hamujakiweza bado. Na hata sasa hamukiwezi, kwa sababu mungali munatawaliwa na mambo ya kidunia. Kwa maana ikiwa kungali wivu na ugomvi katikati yenu, haionyeshi kwamba munatawaliwa na mambo ya kidunia, nanyi munaishi kufuatana na hali ya kimutu? Wakati mumoja wenu anaposema: “Mimi ni wa Paulo” na mwingine anasema: “Mimi ni wa Apolo,” basi ninyi hamufanyi mambo ya kidunia? Basi, Apolo ni nani? Na Paulo ni nani? Sisi ni watumishi wa Mungu, waliowaonyesha ninyi njia ya kuamini. Tumefanya vile kila mumoja wetu kwa kadiri ya zawadi aliyopewa na Bwana. Mimi nilipanda mbegu na Apolo alinyweshea maji, lakini Mungu ndiye aliyeiotesha. Hivi yule anayepanda na yule anayenyweshea maji, wote si kitu; Mungu ndiye anayekuwa wa lazima kwa maana ni yeye anayeotesha mbegu. Yule anayepanda na yule anayenyweshea maji wote ni sawa; naye Mungu atamupa kila mutu mushahara wake kufuatana na kazi aliyofanya. Kwa maana sisi tunashirikiana na Mungu katika kazi, na ninyi ni shamba la Mungu. Vilevile ninyi ni majengo ya Mungu. Kwa kadiri ya zawadi Mungu aliyonipatia, kama vile fundi wa kujenga mwenye hekima, niliweka musingi. Na sasa, mutu mwingine anajenga juu yake. Lakini inafaa kila mutu aangalie vizuri namna anavyojenga. Kwa maana hakuna mutu anayeweza kuweka musingi mwingine pahali pa ule uliokwisha kuwekwa, ni kusema Yesu Kristo. Mutu anaweza kujenga juu ya musingi huu na zahabu, feza, mawe ya bei kali, miti, nyasi au majani. Lakini hali ya kazi ya kila mutu itaonekana wazi, kwa sababu Siku ile ya hukumu itaionyesha waziwazi. Kwa maana Siku ile itajitokeza katikati ya moto, na moto ule ndio utakaopima na kuonyesha hali ya kazi ya kila mutu. Na ikiwa kile mutu alichojenga juu ya musingi huu hakiungui na moto, mutu yule atapokea zawadi. Lakini kama kile alichojenga kikiungua, yeye atakosa zawadi, hata hivi yeye mwenyewe ataokolewa, lakini itakuwa kama vile ameopolewa toka ndani ya moto. Hamujui hakika kuwa ninyi ni hekalu la Mungu na kuwa Roho wa Mungu anakaa ndani yenu? Basi mutu akiharibu hekalu la Mungu, Mungu atamuharibu vilevile. Kwa maana hekalu la Mungu ni takatifu, na ninyi ndilo hekalu lake. Mutu yeyote asijidanganye mwenyewe. Kama mutu fulani kati yenu akijizania kuwa mwenye hekima ya kidunia, ajifanye kama mupumbafu kusudi apate kuwa na hekima ya kweli. Kwa maana hekima ya kidunia ni upumbafu mbele ya Mungu. Ni sawa vile Maandiko Matakatifu yanavyosema: “Mungu anawanasa wenye hekima katika werevu wao wenyewe.” Nayo yanasema vilevile: “Bwana anatambua mawazo ya wenye hekima; anajua kwamba ni ya bure.” Basi mutu asijivune kwa ajili ya wanadamu. Kwa maana vitu vyote ni vyenu: ikiwa Paulo, Apolo au Petro, dunia, uzima, kifo, mambo ya sasa au mambo yatakayokuja. Lakini ninyi ni watu wa Kristo, naye Kristo ni wa Mungu. Kwa hiyo mutuhesabu kama watumishi wa Kristo, wanaoshugulika na ujumbe wa siri wa Mungu. Yanayohitajika kwa mwenye madaraka kama hayo, ni kuwa mwaminifu. Kwa ngambo yangu, si neno hata kidogo kuhukumiwa nanyi au na tribinali ya watu. Na hata mimi mwenyewe sijihukumu. Kweli zamiri yangu hainihukumu juu ya neno lolote, lakini hii si kusema kwamba mimi ni mwenye haki. Bwana ndiye anayenihukumu. Kwa hiyo musihukumu mutu mbele ya wakati uliopangwa; mungojee mpaka Bwana atakaporudia. Yeye ndiye atakayeonyesha wazi katika mwangaza mambo yote yaliyofichwa katika giza na kufunua nia za siri za watu. Halafu kila mutu atapokea sifa anayostahili toka kwa Mungu. Wandugu zangu, nimesema maneno haya nikitwaa mufano wa Apolo na wangu mimi mwenyewe kusudi yakuwe fundisho kwenu. Nilitaka kwamba kufuatana na mufano huu mujifunze maana ya masemi haya: “Musipite pembeni ya maandiko.” Hata mutu mumoja kati yenu asijivunie mutu fulani na kuzarau mwingine. Ni nani aliyekuweka kuwa mukubwa kuliko wengine? Si Mungu ndiye aliyekupa vitu vyote unavyokuwa navyo? Ikiwa ni hivi, kwa sababu gani unajivuna kama vile haukuvipewa kama zawadi? Sasa mumekwisha kupata vyote munavyohitaji! Mumekwisha kuwa watajiri! Munakuwa wafalme ingawa sisi hatuko wafalme. Heri mungekuwa kweli watawala kusudi nasi vilevile tupate kutawala pamoja nanyi. Kwa maana inaonekana kuwa Mungu ametufanya sisi mitume kuwa watu wenye hali ya chini kabisa. Tunahesabiwa kama watu wanaohukumiwa kufa mbele ya watu. Tumewekwa kama kitu cha kushangaza, kinachoangaliwa na dunia nzima, nao wamalaika na watu vilevile. Sisi ni wapumbafu kwa ajili ya Kristo, lakini ninyi ni wenye hekima katika kuungana kwenu na Kristo. Sisi ni zaifu, lakini ninyi ni wenye nguvu. Tunazarauliwa, lakini ninyi munaheshimiwa! Hata sasa, tunateswa na njaa na kiu, tunakosa nguo, tunapigwa, tunatangatanga bila makao. Tunasumbuka sana tukifanya kazi kwa mikono yetu wenyewe. Wakati tunapotukanwa, tunabariki; wakati tunapoteswa, tunavumilia; wakati tunaposingiziwa, tunajibu kwa upole. Hata sasa tunahesabiwa kama takataka za dunia, na kila mutu anatuangalia kama uchafu. Siwaandikii maneno haya kwa kuwapatisha haya, lakini kwa kuwaonya kama watoto wangu wapendwa. Hivi kuelekea maisha yenu na Kristo, hata mukiwa na walezi maelfu muko tu na baba mumoja. Kwa maana kuelekea maisha yenu na Yesu Kristo ni mimi niliyewazaa kwa njia ya kuwatangazia Habari Njema. Basi ninawasihi, mufuate mufano wangu. Ni kwa sababu hii ninawatumia ninyi Timoteo. Yeye ni mwana wangu mupendwa na mwaminifu mbele ya Bwana. Atawakumbusha kanuni ninazofuata katika maisha yangu na Yesu Kristo, nami ninazofundisha fasi zote katika makanisa yote. Watu wamoja kati yenu wanajivuna wakifikiri kwamba sitakuja kuwaona. Lakini nitakuja kwenu upesi Bwana akitaka. Basi pale nitajua maneno ya wale wanaojivuna na kujionea uwezo wao vilevile! Kwa maana kazi ya Ufalme wa Mungu haionyeshwi kwa njia ya kusema tu, lakini vilevile kwa njia ya matendo ya uwezo. Basi munataka nini? Nifike kule kwenu, nikikuja na fimbo au na moyo unaojaa upendo na upole? Habari inasikilika fasi zote kwamba kunafanyika uzinzi katikati yenu. Wanaeleza kwamba uzinzi huu ni ubaya mukubwa, usiofanyika hata katikati ya wapagani, kwa maana wanasema kwamba kuna mumoja wenu ambaye amekamata muke wa baba yake kuwa muke wake! Nanyi munajaa na kiburi. Ninyi mungepaswa kuhuzunika na mutu yule aliyefanya kile kitendo, naye angepaswa kutengwa toka katikati yenu. Basi munapaswa kumutoa mutu yule kwa Shetani, kusudi mwili wake uharibiwe, nayo roho yake iweze kuokolewa Siku ile Bwana Yesu atakaporudi. Hamuna kitu cha kujivunia! Hamujui vizuri mufano unaosema kwamba chachu kidogo inachachisha donge zima? Basi mujitakase, mukiondoa ile chachu ya zamani ya zambi. Hivi mutakuwa kama donge jipya, lisilotiwa chachu, sawa vile munavyokuwa kwa kweli. Mufanye vile kwa maana Kristo amekwisha kutolewa sadaka kwa ajili yetu kama vile kondoo wa Pasaka. Kwa hiyo tufanye karamu yetu ya Pasaka pasipo kutumia mikate iliyotiwa chachu; ni kusema pasipo zambi na uovu. Lakini tutumie mikate isiyotiwa chachu; ni kusema katika usafi na ukweli. Katika barua niliyowatumia, niliwaandikia kwamba musishirikiane na washerati. Hiyo sikusema kabisa kwamba musishirikiane na wote wanaokuwa wazinzi katika dunia hii, wala wenye tamaa, wala wanyanganyi, wala wenye kuabudu sanamu. Kwa maana kwa kujitenga nao, ingewapasa kutoka katika dunia! Lakini niliwaandikia kwamba musishirikiane na mutu anayejiita ndugu mwamini, akiwa mwasherati, mwenye tamaa, mwenye kuabudu sanamu, mutukanaji, mulevi au munyanganyi. Na zaidi ya ile musichangie chakula na mutu wa namna hii. Wakati mutu mumoja kati yenu anapokuwa na ugomvi na ndugu mwenzake mwamini, atasubutu namna gani kwenda kumushitaki mbele ya waamuzi wapagani pahali pa kumushitaki mbele ya watu wa Mungu? Hamujui kwamba watu wa Mungu ndio watakaohukumu dunia? Na kama ikiwapasa kuhukumu dunia, hamuwezi hata kuhukumu mambo ya burebure? Ninyi hamujui kwamba tutawahukumu wamalaika? Basi, ninyi munaweza kuhukumu zaidi mambo ya maisha haya! Basi ikiwa muna magomvi juu ya mambo ya namna hii, kwa nini munayapeleka mbele ya waamuzi wasiokuwa na madaraka katika kanisa? Ninasema hivi kwa kuwapatisha haya. Hakika kati yenu hakuna hata mutu mumoja mwenye hekima anayeweza kukata maneno kati ya wandugu zake waamini? Lakini sasa ndugu mwamini anamushitaki mwenzake mbele ya waamuzi wasioamini. Kweli mambo haya ya kuwa na mashitaki kati yenu yanahakikisha kwamba mumeshindwa kabisa. Si ingekuwa vizuri zaidi kwenu kuvumilia ubaya? Si ingekuwa vizuri zaidi kunyanganywa mali zenu? Lakini, ni ninyi ndio munaotenda vibaya na kunyanganya mali ya wengine, nao munaowatendea vile ni wandugu zenu waamini. Ninyi munajua hakika kwamba watenda mabaya hawatapata urizi katika Ufalme wa Mungu. Musidanganyike: waasherati, wenye kuabudu sanamu, wazinzi, waasherati wa muke kwa muke na mume kwa mume, wizi, wenye tamaa, walevi, watukanaji, wanyanganyi, watu wale wote hawatapata urizi katika Ufalme wa Mungu. Na wamoja kati yenu walikuwa kama wao. Lakini mumesafishwa toka zambi, mumetakaswa na kuhesabiwa haki mbele ya Mungu kwa jina la Bwana Yesu Kristo na kwa Roho wa Mungu wetu. Wamoja kati yenu wanasema: “Vitu vyote vinaruhusiwa kwangu.” Ndiyo, lakini vyote si vyenye kufaa kwenu. Ninaweza kusema kwamba vitu vyote vinaruhusiwa kwangu, lakini sitakubali kuwa mutumwa wa kitu chochote. Nanyi munasema vilevile: “Chakula kiliumbwa kwa ajili ya tumbo nayo tumbo kwa ajili ya chakula.” Ndiyo, lakini Mungu ataharibu vyote viwili. Lakini mwili haukuumbwa kwa ajili ya uasherati. Mwili uliumbwa kwa ajili ya Bwana nao ni wake. Mungu aliyemufufua Bwana Yesu atatufufua nasi vilevile kwa uwezo wake. Munajua kwamba miili yenu ni viungo vya mwili wa Kristo. Basi nitatwaa kiungo cha mwili wa Kristo kwa kukifanya kuwa kiungo cha kahaba? Hapana hata kidogo! Au hamujui kwamba mutu yule anayeungana na kahaba amekwisha kuwa mwili mumoja naye? Kwa maana Maandiko Matakatifu yanasema: “Hao wawili watakuwa mwili mumoja.” Lakini anayeungana na Bwana anageuka kuwa mumoja naye kiroho. Muepuke uzinzi! Zambi ingine yoyote mutu anayofanya haigusi mwili wake, lakini yule anayefanya uzinzi anafanya zambi juu ya mwili wake mwenyewe. Hamujui kwamba mwili wenu ni hekalu la Roho Mutakatifu anayekuwa ndani yenu, yule muliyepewa na Mungu? Na ninyi si mali yenu wenyewe. Kwa sababu mulinunuliwa na Mungu kwa bei kali. Basi mutumie miili yenu na roho zenu kwa utukufu wa Mungu. Sasa tuangalie mambo yale muliyoniandikia. Ni vizuri mwanaume asioe. Lakini kwa ajili ya kuepuka uasherati inafaa kila mwanaume akuwe na muke wake wa pekee, na kila mwanamuke akuwe na mume wake wa pekee. Mume anapaswa kumutimizia muke wake mapaswa yake, na muke anapaswa kumutimizia mume wake mapaswa yake. Muke hawezi kuamua sawa anavyotaka juu ya mwili wake mwenyewe; kwa sababu ni mwili wa mume wake. Vilevile mume hawezi kuamua sawa anavyotaka juu ya mwili wake mwenyewe; kwa sababu ni mwili wa muke wake. Musinyimane, isipokuwa tu mumepatana na kwa muda tu kusudi mupate wakati wa kujitoa kwa kufunga na kuomba. Kisha munaweza kurudiliana tena kusudi Shetani asiwajaribu katika uzaifu wenu. Maneno hayo ninayowaambia si amri, lakini ni ruhusa tu ninayowapa. Hakika, ningetamani watu wote wakuwe kama mimi, lakini kila mutu amepewa zawadi yake ya kipekee na Mungu, mumoja zawadi hii, na mwingine zawadi ile. Na kwa wale wasiooa bado na wajane, ninawaambia kwamba ingekuwa vema waendelee kuishi peke yao kama vile mimi. Lakini kama hawawezi kujizuiza wao wenyewe, basi waoane; kwa maana afazali kuoa kuliko kuwaka tamaa. Kwa wale waliokwisha kuoana, ninatoa amri hii, isiyotoka kwangu, lakini kwa Bwana Mungu: muke hapaswi kuachana na mume wake. Lakini kama muke akiachana na mume wake, asiolewe tena, kama si vile apatane tena na mume wake. Vilevile mume hapaswi kufukuza muke wake. Na kwa wengine, mimi ninawaambia maneno haya, lakini hayatoki kwa Bwana: kama mume mwamini akiwa na muke asiyeamini, naye muke yule akikubali kuishi pamoja naye, asimufukuze. Vilevile kama muke mwamini akiwa na mume asiyeamini, naye mume yule akikubali kuishi pamoja naye, asiachane na mume wake. Kwa maana, mume asiyeamini anapata ushirika na Mungu kwa njia ya kuungana kwake na muke wake. Vilevile muke asiyeamini anapata ushirika na Mungu kwa njia ya kuungana kwake na mume wake. Kama isingekuwa vile, watoto wao wangehesabiwa kama watoto wa wapagani, lakini kwa hakika wao ni watu wa Mungu. Lakini kama mume au muke mupagani akitaka kuachana na mwamini aliyeoana naye, aachane naye. Katika mambo kama hayo, ndugu au dada mwamini yuko huru, kwa maana Mungu amewaita kusudi mukae katika amani. Wewe muke mwamini unaweza kujua namna gani kwamba utamwokoa mume wako? Au wewe mume mwamini utaweza kujua namna gani kwamba utamwokoa muke wako? Kwa ngambo ingine, kila mutu aendelee kuishi kufuatana na zawadi aliyopewa na Bwana na kufuatana na vile alivyokuwa mbele ya kuitwa na Mungu. Hii ndiyo kanuni ninayofundisha katika makanisa yote. Ikiwa mutu alitahiriwa mbele ya kuitwa na Mungu, asitafute kufuta kovu la kutahiriwa kwake. Ikiwa alikuwa hajatahiriwa wakati alipoitwa na Mungu, hapaswi kutahiriwa. Kutahiriwa au kutotahiriwa hakufai kitu. Kitu kinachofaa ni kutii amri za Mungu. Inafaa kila mutu abaki sawa alivyokuwa wakati alipoitwa na Mungu. Ikiwa ulikuwa mutumwa wakati Mungu alipokuita, usihuzunike. Lakini ikiwa kuna bahati ya kupata uhuru, usiipoteze bure. Kwa maana mutumwa aliyeitwa kuwa wa Bwana, amepewa uhuru na Bwana. Hivi vilevile mutu mwenye uhuru aliyeitwa na Kristo, ni mutumwa wa Kristo. Mumenunuliwa na Mungu kwa bei kali, basi musikuwe tena watumwa wa watu. Wandugu zangu, inafaa kila mutu akae katika ushirika wake na Mungu akibaki sawa alivyokuwa wakati alipoitwa naye. Kuelekea wale ambao hawajaoa wala kuolewa, sina neno la kuwaamuru kutoka kwa Bwana. Lakini nitawatolea shauri kufuatana na vile ninavyokuwa mutu anayestahili kuaminiwa, kutokana na neema niliyopewa na Bwana. Kwa sababu ya taabu ya siku hizi, ninafikiri kwamba ni vizuri mutu akae sawa vile anavyokuwa. Ikiwa umekwisha kuoa, usitafute kuachana na muke wako. Lakini kama ukioa, haufanyi zambi, na kama binti anaolewa, yeye hafanyi zambi vilevile. Lakini wale wanaooana watakuwa na mateso katika maisha yao, na mimi ninataka kuwaonya kusudi muepuke mateso yale. Wandugu zangu, mimi ninataka kusema hivi: wakati uliopangwa unabaki mufupi. Tangu sasa wale waliooa waishi kama vile wasiooa. Wale wanaolia wakuwe kama vile wasiolia. Wale wanaofurahi wakuwe kama vile wasiofurahi. Wale wanaonunua vitu wakuwe kama vile hawana kitu. Wale wanaotumia mali ya dunia hii wakuwe kama vile wasioitumia. Kwa maana dunia hii inakaribia kupita. Ningependa muishi bila masumbuko yoyote. Mutu asiyeoa anashugulikia mambo ya Bwana, anatafuta jinsi ya kumupendeza Bwana. Lakini mutu aliyeoa anasumbukia mambo ya dunia, anatafuta jinsi ya kupendeza muke wake. Yeye anashugulikia mambo mawili. Vilevile mwanamuke asiyeolewa au binti anashugulikia mambo ya Bwana. Anajitolea kwa Bwana katika mawazo na matendo yake yote. Lakini mwanamuke anayeolewa, anashugulikia mambo ya dunia, anatafuta jinsi ya kumupendeza mume wake. Maneno hayo ninayosema ni kwa faida yenu, wala si kwa kuwafungia njia. Ninataka kuwaonyesha namna ya kuishi sawa inavyofaa, kusudi mupate kumutumikia Bwana pasipo kizuizo chochote. Mutu akiona kwamba hamutendei muchumba wake vizuri, naye akitawaliwa na tamaa kwamba wangepaswa kuoana, basi afanye sawa vile anavyotaka. Yeye hafanyi zambi, waoane tu. Lakini inawezekana kwa mutu yule kuchunga kusudi lake bila kushurutishwa. Akiweza kutimiza sawa na mapenzi yake, akiamua kwamba hataki kumwoa muchumba wake, basi yeye anafanya vizuri kutomwoa. Hivi yule anayemwoa muchumba wake anafanya vizuri, na yule anayekataa kumwoa muchumba wake, anafanya vizuri zaidi. Mwanamuke aliyeolewa anafungwa na Sheria katika maisha yake na mume wake wakati mume wake angali muzima. Lakini kama mume wake akikufa, yeye ni huru kuolewa na yule anayetaka, lakini sherti ndoa ikuwe ya kikristo. Lakini ingekuwa heri zaidi kama angekaa sawa vile anavyokuwa. Hilo ni shauri langu, nami vilevile ninazani kwamba ninaongozwa na Roho wa Mungu. Sasa tuangalie mambo yanayoelekea nyama zinazotolewa kwa kutambikia sanamu za miungu: tunajua kwamba “sisi wote tuko na elimu,” kama vile munavyozoea kusema. Elimu inamufanya mutu kuwa na kiburi, lakini upendo unawajenga watu katika imani. Kama mutu anajizania kwamba anajua kitu, yeye hakijui hakika sawa vile inavyomupasa kukijua. Lakini yule anayemupenda Mungu, huyu anajulikana naye. Basi kuelekea lile ulizo juu ya kula nyama za kutambikiwa kwa sanamu za miungu, tunajua kwamba sanamu ni kitu bure katika dunia, na ya kuwa kuna Mungu mumoja peke yake tu. Kuko wale wanaoitwa miungu katika mbingu na katika dunia, na hivi kuko “miungu” mingi na “wabwana” wengi. Ingawa hivi, kwa ngambo yetu sisi tuko na Mungu mumoja peke yake tu, ndiye Baba aliyeumba vitu vyote, nasi tunaishi kwa nguvu yake. Vilevile kuko Bwana mumoja tu, ndiye Yesu Kristo. Kwa njia yake vitu vyote viliumbwa, nasi tunaishi kwa nguvu yake. Lakini si watu wote wanaofahamu mambo hayo. Wengi wamezoea kutambikia sanamu za miungu mpaka sasa, wanakula nyama wakizihesabu hakika kuwa za kutambikia sanamu zile. Kwa sababu zamiri yao ni mbovu, wanajisikia kwamba wanajichafua kwa kula chakula kile. Chakula hakitaleta ushirika kati yetu na Mungu. Kama tukiacha kula hatupungukiwi kitu na kama tukikula hatuongezewi kitu. Lakini, muangalie vizuri kusudi uhuru wenu usiangushe wale wanaokuwa zaifu katika imani. Kwa maana kama mutu zaifu katika imani akikuona wewe mwenye elimu unakula katika hekalu la sanamu, si zamiri yake itamusukuma kula vyakula vya kutambikia sanamu? Na hivi kwa sababu ya elimu yako, yule ndugu mwamini zaifu ambaye Kristo alikufa kwa ajili yake, atapotea. Kwa kuwakosesha wandugu zenu kama hivi na kuumiza zamiri yao, ni kama vile munamukosea Kristo mwenyewe. Kwa hiyo chakula kikimwangusha ndugu yangu katika zambi, nitajizuiza kula nyama siku zote kusudi nisimwangushe ndugu yangu. Mimi si huru? Mimi si mutume? Mimi sikumwona Yesu Kristo Bwana wetu? Ninyi si matunda ya kazi yangu kwa ajili ya Bwana? Hata ikiwa watu wengine hawakubali kuwa mimi ni mutume, ninyi munakubali kuwa mimi ni mutume. Ninyi ni kitambulisho kinachohakikisha kwamba mimi ni mutume, kwa ajili ya kuungana kwenu na Bwana. Watu wanaponishitaki, mimi ninajitetea kwa namna hii: basi sina haki ya kupokea chakula na kinywaji kwa ajili ya kazi yangu? Au sina haki ya kusafiri pamoja na mwanamuke mukristo kama vile mitume wengine wanavyofanya, nao wandugu za Bwana na hata Petro? Au ni mimi na Barnaba tu ndio tunaopaswa kujitumikia wenyewe kwa kupata vifaa vya maisha? Ni askari gani anayejilipia mwenyewe vifaa vya kiaskari? Au ni muchungaji gani asiyekunywa maziwa ya kundi analochunga? Musifikiri kuwa ninasema maneno hayo kufuatana na mambo ya maisha. Hata Sheria ya Musa inasema maneno hayo vilevile. Kwa maana imeandikwa hivi katika Sheria ile: “Usifunge kinywa cha ngombe anapokanyaga ngano.” Mungu anashugulikia ngombe? Hasemi maneno haya zaidi sana kwa ajili yetu? Hakika, maneno hayo yaliandikwa kwa ajili yetu. Inafaa yule anayelima na yule anayetwanga watumike wakiwa na tumaini la kupata sehemu yao ya mavuno. Ikiwa tumepanda mbegu ya kiroho ndani yenu, basi kuna jambo gani kubwa kama nasi tukitazamia kupata vifaa vya kimwili toka kwenu? Ikiwa wengine wako na haki ya kupata vitu kama vile toka kwenu, sisi hatuna haki zaidi kuliko wao? Sisi hatudai kutendewa sawa na haki yetu, lakini tunavumilia kusudi tusiiwekee Habari Njema ya Kristo kizuizo chochote. Munajua hakika kuwa wale wanaotumika katika hekalu wanapata chakula chao ndani ya hekalu. Na wale wanaotumika kwa kutoa sadaka juu ya mazabahu wanapata sehemu yao kutoka sadaka zile. Vilevile, Bwana aliagiza kuwa wale wanaohubiri Habari Njema wanapaswa kuishi kwa njia ya Habari Njema. Lakini mimi sikudai hata neno moja ya haki hizo, wala sikuandikii haya kwa kusudi la kutafuta kuzipewa. Ingekuwa heri kwangu kufa kuliko kuzuizwa na mutu yeyote kwamba nisijisifu juu ya jambo hili. Mimi sina haki ya kujisifu kwa sababu ninatangaza Habari Njema, kwa maana nimelazimishwa kuitangaza. Basi ole kwangu kama nisipotangaza Habari Njema. Ingekuwa nimechagua kazi hii kwa mapenzi yangu mwenyewe, ningeweza kungojea kupokea mushahara. Lakini kwa kuwa ni muzigo niliopewa, inanipasa kuitimiza. Basi mushahara wangu ni gani? Mushahara wangu ni kutangaza Habari Njema bila kulipwa, maana yake bila kudai haki ninazostahili kwa kuitangaza. Mimi si mutumwa wa mutu yeyote. Lakini nimejifanya kuwa mutumwa wa watu kusudi nipate wengi kati yao sawa inavyowezekana. Kwa Wayuda, ninaishi kama Muyuda, kusudi niwapate Wayuda. Mimi siishi chini ya uongozi wa Sheria ya Musa, lakini kusudi niwapate wale wanaoishi chini ya Sheria ile, ninapokuwa kati yao, ninaishi kufuatana na Sheria ile. Vilevile ninapokuwa kati ya wasioishi chini ya Sheria ya Musa, ninaishi kama wao, bila kuangalia Sheria, kusudi niwapate. Hii si kusema kwamba mimi sishiki sheria ya Mungu, kwa maana mimi ni chini ya uongozi wa sheria ya Kristo. Na kwa wale wanaokuwa zaifu katika imani, ninajifanya kama muzaifu kusudi niwapate hao wanaokuwa zaifu. Kwa wote nimejifunza kuwa mwenye hali kama yao, kusudi nipate kuokoa wamoja kati yao kwa njia mbalimbali. Ninafanya hayo yote kwa ajili ya Habari Njema kusudi nipate sehemu ya baraka zake. Munajua hakika kuwa wale wanaofanya mashindano ya kukimbia, wote wanakimbia lakini ni mumoja tu anayepokea zawadi. Basi mukimbie hata mufikie kupokea zawadi. Na kila mutu anayefanya mashindano katika michezo anajizuiza na vitu vingi katika mazoezi yake. Basi wanafanya hivi kusudi wapate taji yenye kuharibika; lakini sisi tunafanya vile, kusudi tupate taji isiyoharibika. Ni kwa sababu hiyo ninakimbia nikiwa na shabaha ya kushinda. Mimi ni kama mupiganaji wa ngumi asiyepiga katika hewa. Lakini ninatesa mwili wangu kwa mazoezi makali na kuutumikisha vikali kusudi mimi mwenyewe nisikataliwe kisha kutangaza ujumbe kwa watu wengine. Wandugu zangu, ninataka mukumbuke kwamba babu zetu wote walisafiri wakiongozwa na wingu, nao wote walivuka katikati ya bahari Nyekundu kwa usalama. Wote walibatizwa katika lile wingu na katika ile bahari kusudi wapate kuungana na Musa. Wote walikula chakula kimoja cha kiroho. Wote walikunywa kinywaji kimoja cha kiroho; kwa maana walikunywa maji yaliyotoka ndani ya lile jiwe lililosafiri pamoja nao, nalo jiwe lilikuwa Kristo. Lakini, wengi sana kati yao hawakumupendeza Mungu, kwa hiyo wakakufia katika jangwa. Mambo hayo ni mufano kwetu, kusudi tusikuwe na tamaa mbaya kama vile wao. Basi musikuwe wenye kuabudu sanamu kama wamoja kati yao walivyokuwa; kama vile Maandiko haya Matakatifu yanavyosema: “Watu wakaikaa kula na kunywa na kisha wakasimama kwa kujifurahisha.” Musifanye uasherati kama vile wamoja kati yao walivyofanya hata wakakufa kwa siku moja watu elfu makumi mbili na tatu. Vilevile tusimupime Bwana kama vile wamoja wao walivyofanya, hata wakauawa na nyoka. Musinungunike kama vile wamoja kati yao walivyofanya hata malaika mwangamizaji akawateketeza. Mambo haya yote yaliwafikia kusudi yakuwe mufano kwa watu wengine; yameandikwa kwa kutuonya sisi, kwa maana tunaishi katika kipindi cha mwisho wa nyakati. Kwa hiyo yule anayefikiri kwamba anasimama imara, afanye angalisho asianguke. Majaribu yale munayopata, ni yale yanayowapata watu wengine wote. Mungu hatawaachilia kujaribiwa kupita nguvu zenu, kwa maana yeye ni mwaminifu. Jaribu litakapowatokea, atawapatia nguvu ya kulivumilia, hata muweze kulishinda. Kwa hiyo wapenzi wangu, muepuke kutambikia sanamu. Ninasema nanyi kama watu wenye akili; muamue ninyi wenyewe juu ya maneno ninayotaka kuwaambia: tunapokunywa kikombe ambacho kwa ajili yake tunamutolea Mungu shukrani, basi kwa njia ya kikombe kile hatuungani na damu ya Kristo? Nasi tunapomega mukate na kuukula, kwa njia hiyo, mukate ule hautuungi na mwili wa Kristo? Kwa kuwa mukate ni mumoja, ijapokuwa sisi ni wengi, tuko mwili mumoja, kwa maana sisi wote tunashiriki mukate ule mumoja. Muangalie mufano wa Waisraeli: wale wanaokula vitu vinavyotolewa sadaka juu ya mazabahu wanaungana na Mungu kwa njia ya sadaka ile. Basi niseme nini? Nyama iliyotambikiwa kwa sanamu ni yenye mafaa? Au kwamba sanamu ni kitu cha lazima? Hapana. Ninataka kusema kwamba vitu wapagani wanavyotambikia, wanavitolea pepo wala si Mungu. Nami sipendi mushirikiane na pepo hata mara moja. Hamuwezi kuchangia kikombe cha Bwana na kikombe cha pepo. Vilevile hamuwezi kuchangia meza ya Bwana na meza ya pepo. Au tunataka kumuchokoza Bwana hata asikie wivu? Munafikiri kuwa sisi tuko na nguvu kuliko yeye? Wamoja wenu wanasema: “Vitu vyote vinaruhusiwa.” Ni kweli, lakini vyote havifai. “Vitu vyote vinaruhusiwa,” lakini vyote havifai kwa kujenga imani. Mutu asitafute faida yake mwenyewe, lakini faida ya mwenzake. Ninyi ni huru kwa kula kila kitu kinachouzishwa katika soko bila kuulizauliza neno kwa sababu ya zamiri. Kwa maana Maandiko Matakatifu yanasema: “Dunia na vyote vinavyokuwa ndani yake ni vya Bwana.” Kama mupagani anawaalika kula chakula, nanyi mukikubali kwenda kule, mukule vyote wanavyotoa kwenu bila kuulizauliza neno kwa sababu ya zamiri. Lakini kama mutu akiwaambia ninyi: “Vyakula hivi vimetambikiwa kwa sanamu,” basi musivikule kwa ajili ya yule aliyewaarifu na kwa ajili ya zamiri. Sisemi juu ya zamiri zenu, lakini juu ya zamiri ya yule aliyewaarifu. Labda kuna mutu anayeweza kuuliza: “Kwa sababu gani ninaweza kuzuizwa kutenda sawa na uhuru wangu kwa ajili ya mwingine? Kama ninamushukuru Mungu kwa ajili ya chakula ninachokula, kwa nini wananiteta juu ya chakula ambacho kwa ajili yake ninamutolea Mungu shukrani?” Basi, kama mukikula au mukikunywa, au mukifanya neno lolote, mufanye yote kwa ajili ya utukufu wa Mungu. Basi muangalie, kusudi musiwakwaze Wayuda, wala wasiokuwa Wayuda, wala kanisa la Mungu. Mufanye kama vile mimi: ninajikaza kwa kupendeza watu wote katika mambo yote, maana sitafuti faida yangu mimi mwenyewe, lakini faida ya watu wote, kusudi waokolewe. Mufuate mufano wangu kama vile mimi ninavyofuata mufano wa Kristo. Ninawashukuru kwa sababu munanikumbuka katika mambo yote na kwa sababu munashika mafundisho yangu sawa vile nilivyoyafundisha kwenu. Lakini ninataka mufahamu maneno haya: Kristo ni kichwa cha kila mwanaume, na mwanaume ni kichwa cha muke wake, na Mungu ni kichwa cha Kristo. Basi mwanaume yeyote akifunika kichwa chake wakati anapoomba Mungu, au anapotabiri, anamuzaraulisha Kristo. Lakini mwanamuke yeyote asipofunika kichwa chake wakati anapoomba au anapotabiri, anamuzaraulisha mume wake. Tendo hilo linahesabiwa kama vile amenyolewa. Kama mwanamuke hafuniki kichwa, anaweza basi kunyolewa! Lakini kwa sababu ni haya kwa mwanamuke kukatwa nywele au kunyolewa, basi inafaa afunike kichwa. Mwanaume hapaswi kufunika kichwa, kwa sababu yeye ni mufano na utukufu wa Mungu. Lakini mwanamuke ni utukufu wa mwanaume. Kwa maana mwanaume hakuumbwa kutoka katika mwanamuke, lakini mwanamuke aliumbwa kutoka katika mwanaume. Na zaidi ya hii, mwanaume hakuumbwa kwa ajili ya mwanamuke, lakini mwanamuke aliumbwa kwa ajili ya mwanaume. Kwa hiyo, kwa sababu ya wamalaika, mwanamuke anapaswa kufunika kichwa chake kuwa kitambulisho kinachoonyesha kuwa yuko chini ya mamlaka ya mume wake. Lakini katika ushirika wetu na Bwana, hakuwezi kuwa mwanamuke pasipo mwanaume wala mwanaume pasipo mwanamuke. Kwa maana kama vile mwanamuke alivyoumbwa kutoka katika mwanaume, vilevile mwanaume anazaliwa na mwanamuke; na vyote vinatoka kwa Mungu. Muamue ninyi wenyewe: ni vema mwanamuke asifunike kichwa anapoomba Mungu wakati wa ibada? Hali ya asili yenyewe inawaonyesha kuwa ni haya kwa mwanaume kuwa na nywele ndefu, lakini ni heshima kwa mwanamuke kuwa na nywele ndefu. Kwa maana nywele ndefu zimetolewa kwa mwanamuke kwa kuwa nguo ya kufunika kichwa. Lakini kama mutu akitaka kubishana juu ya neno hili, ajue kwamba sisi wala makanisa ya Mungu hatuna desturi ingine. Kuelekea maonyo yanayofuata, mimi siwasifu. Kwa maana munapokusanyika, mikutano yenu haiwafalii, lakini inawaletea hasara. Kwanza, ninasikia kwamba munapokusanyika kuna matengano katikati yenu, nami ninasadiki kwamba nusu ya maneno yale ni ya kweli. (Inafaa kuwe matengano kati yenu, kusudi wale wanaokuwa waaminifu wa kweli kati yenu wajulikane.) Munapokusanyika hamukuli karamu ya Bwana. Kwa maana munapokula, kila mumoja anajiharikisha kula chakula chake mwenyewe, hivi wamoja wenu wanasikia njaa na wengine wanalewa. Basi, ninyi hamuna nyumba munamoweza kukulia na kukunywea? Au munazarau kanisa la Mungu na munataka kuwapatisha haya wale wasiokuwa na kitu? Munataka niwaambie ninyi nini? Inafaa niwasifu? Hapana, siwezi kuwasifu hata kidogo juu ya jambo hilo! Kwa maana haya ndiyo mafundisho niliyopokea kutoka kwa Bwana, nami niliyotoa kwenu: katika usiku ule Bwana Yesu alipotolewa, alitwaa mukate, na alipokwisha kumushukuru Mungu, akaumega akisema: “Huu ni mwili wangu unaotolewa kwa ajili yenu. Mufanye hivi kwa kunikumbuka.” Vilevile, nyuma ya kula akatwaa kikombe na kusema: “Kikombe hiki ni agano jipya la Mungu, linalohakikishwa kwa njia ya damu yangu. Mufanye hivi kwa kunikumbuka kila mara munapokikunywa.” Kwa sababu kila mara munapokula mukate huu na kunywa kikombe hiki, munatangaza kufa kwa Bwana mpaka atakapokuja. Basi kila mutu anayekula mukate wa Bwana au kunywa kikombe chake bila kustahili, anafanya zambi akikosea mwili na damu ya Bwana. Basi kila mutu ajichunguze mwenyewe na kisha akule mukate huu na kunywa kikombe hiki. Kwa maana mutu akikula mukate na kunywa kikombe pasipo kutambua maana ya mwili wa Bwana, anajiletea azabu yeye mwenyewe kwa kula na kunywa. Na kwa sababu hii wengi kati yenu ni wagonjwa na wazaifu, na wengi wamekufa. Lakini tungejichunguza sisi wenyewe kwanza, hatungehukumiwa na Mungu. Lakini tunahukumiwa na kuazibiwa na Bwana kusudi tusiazibiwe pamoja na watu wa dunia hii. Kwa hiyo wandugu zangu, wakati munapokusanyika kwa kula karamu ya Bwana, sherti mungojeane. Kama mutu akiwa na njaa, akule katika nyumba yake, kusudi musikusanyike kwa kujiletea azabu. Basi maneno mengine yanayobaki nitayatengeneza wakati nitakapofika kwenu. Sasa tuangalie mambo yanayoelekea zawadi za Roho Mutakatifu. Wandugu zangu, sitaki mukose kufahamu ukweli wa zawadi hizi. Munajua kwamba wakati mulipokuwa wapagani, mulikuwa mukivutwa na kupotoshwa na sanamu zisizosema. Kwa sababu hii ninataka mufahamu kwamba hakuna mutu ambaye anaongozwa na Roho wa Mungu anayeweza kusema: “Yesu alaaniwe,” na hakuna mutu anayeweza kusema: “Yesu ni Bwana,” kama asipoongozwa na Roho Mutakatifu. Kuna zawadi mbalimbali, lakini ni Roho mumoja anayezitoa. Kuna utumishi wa namna mbalimbali, lakini ni Bwana mumoja ndiye wanayemutumikia. Kuna kazi za namna mbalimbali, lakini Mungu ni mumoja anayewezesha watu wote kuzitimiza. Na kwa kila mutu Roho anajifunua kwa faida ya wote. Basi mutu mumoja anapewa na Roho uwezo wa kusema maneno ya hekima, na mwingine uwezo wa kusema maneno ya ufahamu na Roho yule yule. Mwingine anapewa imani na Roho yule yule na mwingine uwezo wa kuponyesha wagonjwa. Mwingine anapewa uwezo wa kufanya miujiza, mwingine zawadi ya kutabiri, na mwingine uwezo wa kutambua roho ya uongo na Roho wa ukweli. Mwingine alipewa uwezo wa kusema luga za ajabu na mwingine uwezo wa kutafsiri luga zile. Ni yule yule Roho mumoja anayetenda mambo hayo yote, akimupa kila mumoja zawadi mbalimbali kama anavyopenda. Kwa maana, Kristo ni kama mwili mumoja unaokuwa na viungo vingi. Ijapokuwa viungo vya mwili ni vingi, vinakuwa mwili mumoja tu. Vilevile sisi wote, Wayuda na watu wa mataifa mengine, watumwa na watu wanaokuwa huru, tumebatizwa kwa Roho mumoja kusudi tukuwe mwili mumoja na sisi wote tumekunyweshwa Roho mumoja. Mwili hauundwi na kiungo kimoja tu, lakini na viungo vingi. Kama muguu ungesema: “Kwa sababu mimi si mukono, basi mimi si wa mwili,” hata vile haungeacha kuwa kiungo cha mwili. Na kama sikio lingesema: “Kwa sababu mimi si jicho, basi mimi si wa mwili,” hata vile halingeacha kuwa kiungo cha mwili. Kama mwili wote ungekuwa jicho, namna gani ungeweza kusikia? Na kama ungekuwa sikio, namna gani ungeweza kunusa? Lakini sasa, Mungu amepanga viungo vya mwili kila kimoja kama ilivyomupendeza. Kama vyote vingekuwa kiungo kimoja, mwili haungekuwa! Kwa hivi sasa kunakuwa viungo vingi lakini mwili ni mumoja. Jicho haliwezi kuuambia mukono: “Sina lazima yako!” Wala kichwa hakiwezi kuiambia miguu: “Sina lazima yenu!” Lakini zaidi ya hiyo, viungo vya mwili vinavyoonekana kuwa zaifu, ndivyo vinavyokuwa vya lazima. Tena viungo vile tunavyozania kwamba havistahili heshima kubwa ndivyo tunavyoheshimu zaidi. Na viungo vinavyokuwa vya haya ndivyo tunavyotunza sana, wakati vile vinavyoheshimiwa havihitaji kitu. Mungu ameunganisha mwili hata akavipatia heshima zaidi viungo vilivyokosa heshima, kusudi kusikuwe mabishano katikati ya viungo vya mwili, lakini vyote visaidiane sawasawa. Kama kiungo kimoja kikiumia, viungo vingine vyote vinaugua pamoja nacho. Kiungo kimoja kikiheshimiwa, viungo vingine vyote vinafurahi pamoja nacho. Ninyi wote ni mwili wa Kristo, na kila mumoja wenu ni kiungo cha mwili ule. Vilevile Mungu ameweka kwanza mitume katika kanisa; pili manabii na tatu walimu; kisha kunakuwa wale wenye zawadi ya kufanya miujiza, ya kuponyesha wagonjwa, ya kusaidia wengine, ya kuongoza wengine, ya kusema luga za ajabu. Wote si mitume, manabii au walimu. Wote hawana uwezo wa kufanya miujiza, wa kuponyesha wagonjwa, wa kusema kwa luga za ajabu, au wa kutafsiri. Basi mutamani sana zawadi inayokuwa bora zaidi. Lakini sasa, nitawaonyesha njia nzuri sana kuliko zote. Hata nikiwa na uwezo wa kusema luga za watu na za wamalaika, lakini kama sina upendo, masemi yangu ni bure kama vile kelele la kengele au matoazi. Hata nikiwa na zawadi ya kutabiri, na uwezo wa kujua mafumbo yote na maarifa yote; hata nikiwa na imani kubwa inayoweza kuhamisha milima; lakini kama sina upendo, mimi ni kitu bure. Ninaweza vilevile kugawanya mali yangu yote kwa kulisha wamasikini na hata kutoa mwili wangu uunguzwe, lakini kama sina upendo, hakuna faida ninayopata. Upendo unavumilia, ni wenye wema; upendo hauna wivu, upendo haujivuni, na hauna kiburi. Upendo haukosi kuwa na adabu, hautafuti faida yake mwenyewe, haukasiriki upesi, nao hauhesabii mutu ubaya. Upendo haufurahii ubaya, lakini unafurahia ukweli. Upendo hauchoki na mambo yote, unaamini mambo yote, unatumaini mambo yote na kuvumilia mambo yote. Upendo haukomi hata kidogo. Lakini kutabiri kunatoweka, zawadi ya kusema kwa luga za ajabu inatoweka, na maarifa yanapita. Kwa maana tunafahamu tu mambo machache na kutabiri tu mambo machache. Lakini wakati mambo matimilifu yatakapokuja, yale yasiokuwa matimilifu yatatoweka. Wakati nilipokuwa mutoto, nilisema kama mutoto, niliwaza kama mutoto, nilifikiri kama mutoto. Lakini nilipokuwa mutu muzima niliacha mambo ya kitoto. Kwa maana wakati wa sasa tunaona kama mwenye kuangalia ndani ya kioo kisichoonyesha wazi, lakini wakati utakaokuja tutaona waziwazi. Kwa sasa ninajua tu mambo machache, lakini nyuma nitajua kwa utimilifu kama vile Mungu anavyonijua mimi. Basi sasa, hivi vitu vitatu vinadumu: imani, tumaini na upendo; lakini kinachokuwa kikubwa kuliko hivi vingine ni upendo. Mujikaze mukuwe na upendo. Vilevile mutamani sana kupata zawadi za Roho, hasa zaidi zawadi ya kutabiri. Mutu anayesema kwa luga ya ajabu hasemi na watu lakini anasema na Mungu, kwa maana hakuna mutu anayemusikia. Kwa uwezo wa Roho, mutu yule anasema mafumbo. Lakini yule anayetabiri anasema na watu maneno ya kuwajenga katika imani, kuwatia moyo na kuwatuliza. Yule anayesema kwa luga ya ajabu anajenga imani yake mwenyewe, lakini yule anayetabiri anajenga imani ya kanisa zima. Ninataka ninyi wote museme kwa luga za ajabu, lakini ninataka zaidi tena mupate kutabiri. Kwa maana, yule anayetabiri ni wa lazima kuliko yule anayesema kwa luga za ajabu, isipokuwa kama huyo mutu anaweza kutafsiri yale anayosema kusudi kanisa zima lijengwe katika imani. Basi wandugu zangu, nitawafalia nini kama nikikuja kwenu na kusema nanyi katika luga za ajabu? Sitawafalia kitu pasipo kuwaelezea maneno ya ufunuo, au ya elimu, pasipo kuwatabiria au kuwafundisha. Tuangalie mufano wa vyombo vya muziki kama vile filimbi au kinanda. Milio ya vyombo hivi isipokuwa mbalimbali, namna gani mutu anavyoweza kutambua wimbo unaopigwa? Ngunga isipopigwa kwa mulio wa kuarifu, askari gani atakayeweza kujitayarisha kwa vita? Ni hivi vilevile mambo munayosema yatatambulikana namna gani ikiwa maneno munayoeleza kwa luga za ajabu hayako wazi? Kwa maana mutakuwa kama wenye kusema na upepo. Kuna namna mbalimbali za luga katika dunia, lakini hakuna hata moja isiyokuwa na maana. Basi kama nisipojua luga fulani, nitakuwa kama mujinga kwa yule anayeisema, naye atakuwa kama mujinga kwangu. Hivi vilevile kufuatana na vile munavyotamani sana zawadi za Roho, mujikaze kupata kwa uwingi zile zinazoweza kujenga kanisa katika imani. Kwa hiyo yule anayesema kwa luga ya ajabu, aombe Mungu amupatie uwezo wa kuitafsiri. Kwa maana kama nikiomba katika luga ya ajabu, roho yangu inaomba, lakini akili yangu haitumiki. Basi ninapaswa kufanya nini? Nitaomba katika roho na katika akili vilevile. Nitaimba katika roho na katika akili vilevile. Kwa maana kama ukimwomba Mungu ndani ya roho tu kwa kumushukuru, mutu asiyeelewa kitu anayehuzuria katika mukutano hawezi kusema amina kwa kuitikia maombi yako ya kushukuru. Ni kwa sababu hasikii mambo unayosema. Ijapokuwa ni kweli maombi yako ya kushukuru yanawezekana kuwa mazuri, lakini hayajengi mutu mwingine katika imani. Ndiyo, ninamushukuru Mungu kwamba ninasema kwa luga za ajabu kuliko ninyi wote. Lakini, katika mukutano ninapenda kusema maneno matano yenye kusikilika, kusudi niwafundishe wengine, kuliko kusema maneno elfu kumi kwa luga za ajabu. Wandugu zangu, musikuwe kama watoto kwa kufikiri: lakini katika mambo mabaya, iwatokee kutenda kama watoto wachanga. Inafaa mafikiri yenu yakuwe kama ya watu wazima. Imeandikwa katika Sheria: “Bwana anasema: ‘Nitasema na watu hawa kwa njia ya wageni wenye luga ngeni Na hata hivi hawatanisikiliza.’ ” Kwa hiyo, zawadi ya kusema luga za ajabu ni kitambulisho kwa wasioamini, lakini si kwa waamini. Na zawadi ya kutabiri ni kitambulisho kwa waamini, lakini si kwa wasioamini. Basi kama kanisa zima limekusanyika, na watu wote wanaanza kusema kwa luga za ajabu; na kisha watu wasioelewa kitu au wasioamini wakiingia katika mukutano wenu hawatasema kuwa ninyi ni wenda-wazimu? Lakini kama wote wakitabiri, na kama mutu mumoja asiyeamini au asiyeelewa kitu anaingia, atapata uhakikisho kutokana na maneno ya hao wote. Naye atahukumiwa kufuatana na yote aliyosikia na kufichuliwa waziwazi mawazo yake aliyoficha. Na hivi atainama uso mpaka chini na kumwabudu Mungu, akisema: “Kweli Mungu ni katikati yenu!” Wandugu zangu, niseme nini basi? Wakati munapokusanyika kwa ibada, mumoja anaweza kuimba wimbo, mwingine kufundisha, mwingine kutoa ufunuo, mwingine kusema kwa luga za ajabu na mwingine anaweza kutafsiri. Na hayo yote yanapaswa kufanyika katika nia ya kujenga kanisa katika imani. Kukiwa wenye kusema kwa luga za ajabu, inafaa wasikuwe zaidi ya wawili au watatu, nao waseme mumoja kwa mumoja. Na tena kunapaswa kuwa mutu wa kutafsiri maneno wanayosema. Kama hakuna mutu anayetafsiri, basi kila mumoja wao anyamaze katika mukutano, aseme tu ndani ya moyo, yeye mwenyewe na Mungu. Na kwa upande wa wale wanaotabiri, wanaweza kusema wawili au watatu na watu wengine wapime yale wanayosema. Lakini kukiwa mutu anayesema, na mwingine anayekaa karibu akipata ufunuo, inafaa yule anayesema anyamaze. Kwa maana ninyi wote munaweza kutabiri mumoja kwa mumoja, kusudi wote wapate kufundishwa na kutiwa moyo. Zawadi ya unabii inapaswa kuwa chini ya utawala wa yule aliyeipewa, kwa maana Mungu hataki sisi tuishi katika fujo, lakini katika amani. Sawa vile inavyokuwa desturi katika makanisa yote ya watu wa Mungu, wanawake wanapaswa kukaa kimya katika mikutano ya kanisa. Wao hawaruhusiwi kusema katika kanisa, lakini wanapaswa kutii sawa vile Sheria inavyosema. Kama wakiwa na neno la kuuliza, waulize waume wao kwenye nyumba zao. Ni haya kwa mwanamuke kusema katika mukutano wa kanisa. Munazani kwamba Neno la Mungu limetoka kwenu au limewafikia ninyi peke yenu tu? Kama mutu akizani kwamba yuko na zawadi ya unabii au zawadi ingine ya Roho, anapaswa kujua kwamba maneno haya ninayowaandikia ninyi ni amri ya Bwana. Lakini kama yeye hajui vile, basi mutu asishugulike naye. Kwa hiyo wandugu zangu, mutamani sana kupata zawadi ya kutabiri, nanyi musiwazuize watu kusema kwa luga za ajabu. Lakini maneno yote yatendeke katika usawa na katika utaratibu. Wandugu zangu, sasa ninataka kuwakumbusha Habari Njema niliyowatangazia, ile muliyopokea na kuishika imara. Nanyi kwa njia ya habari hiyo munaokolewa, ikiwa munaishika kufuatana na maneno niliyowahubiri. Kama isipokuwa hivi, muliamini bure. Kwanza nimewatolea mafundisho haya ambayo mimi mwenyewe nilipokea: Kristo alikufa kwa sababu ya zambi zetu kama vile Maandiko Matakatifu yanavyosema. Alizikwa na kufufuliwa kwa siku ya tatu kisha kufa kwake kama vile Maandiko Matakatifu yanavyosema. Alimutokea Petro, na kisha akawatokea mitume wake kumi na wawili. Nyuma aliwatokea waamini zaidi ya mia tano pamoja, na wengi kati yao wangali wanaishi mpaka sasa, lakini wachache wamekwisha kufa. Kisha alimutokea Yakobo, na nyuma akawatokea mitume wote. Na kwa mwisho wa wote akanitokea mimi vilevile, mimi ninayekuwa kama mutoto aliyezaliwa pasipo kutimiza miezi. Kwa maana mimi ni mudogo kati ya mitume wote, nami sistahili hata kuitwa mutume, kwa maana nilitesa kanisa la Mungu. Lakini kwa neema ya Mungu nimekuwa sawa hivi ninavyokuwa, na neema yake niliyopewa haikukuwa ya bure, lakini nilitumika zaidi sana kuliko mitume wote wengine. Hakika si mimi, lakini ni neema ya Mungu inayokuwa pamoja nami. Basi, ikiwa ni mimi au ikiwa ni wao, hii ndiyo habari tunayohubiri na ndiyo muliyoamini. Ikiwa tunahubiri kuwa Kristo amefufuka, namna gani basi wengine kati yenu wanasema kama wafu hawatafufuka? Basi ikiwa kweli wafu hawatafufuka, Kristo vilevile hakufufuka. Na kama Kristo hakufufuka, mahubiri yetu ni ya bure na kuamini kwenu ni kwa bure vilevile. Na zaidi ya hii, sisi tumeonekana kuwa washuhuda wa uongo mbele ya Mungu, kwa sababu tumeshuhudia kuwa Mungu amemufufua Kristo, ingawa hakumufufua, ikiwa kweli wafu hawafufuki. Kwa maana kama wafu hawafufuki, basi Kristo naye hakufufuka. Na kama Kristo hakufufuka, imani yenu ni ya bure, na mungali katika zambi zenu. Na zaidi ya hii, wale waliokufa wakiamini Kristo wamepotea kabisa. Ikiwa tunamutumainia Kristo juu ya maisha haya ya sasa tu, sisi ni wamasikini kuliko watu wote. Lakini, kwa hakika Kristo amefufuka na hii inahakikisha kwamba wale waliokufa watafufuliwa vilevile. Kwa maana, kama vile kifo kililetwa na mutu mumoja, vilevile ufufuko wa wafu unaletwa na mutu mumoja. Kama vile watu wote wanavyokufa kwa sababu ya kuungana kwao na Adamu, vilevile wote wataishi tena kwa sababu ya kuungana kwao na Kristo. Lakini kila mutu atafufuka kufuatana na utaratibu wake; Kristo ndiye anayekuwa wa kwanza, na kisha watu wake watafufuka, wakati atakaporudia. Na nyuma ya pale, mwisho wa vyote utatimia. Wakati ule Kristo ataharibu utawala wote, mamlaka yote na uwezo wote, naye atamupatia Mungu Baba ufalme. Kwa maana Kristo anapaswa kutawala mpaka atakapowashinda waadui zake wote na kuwaweka chini ya miguu yake. Adui wa mwisho atakayeangamizwa ni kifo. Kwa maana Maandiko Matakatifu yanasema: “Mungu aliweka vitu vyote chini ya miguu yake.” Ndiyo Maandiko Matakatifu yanasema kwamba alipewa mamlaka juu ya vitu vyote. Lakini maneno haya yanaonyesha wazi kwamba Mungu hahesabiwi katika hili neno “Vyote”, kwa maana ni yeye aliyemupa mamlaka juu ya vitu vyote. Na wakati vitu vyote vitakapokuwa vimewekwa chini ya mamlaka ya Mwana, halafu yeye mwenyewe atajiweka chini ya mamlaka ya Mungu aliyemupa mamlaka juu ya vitu vyote, kusudi Mungu apate kutawala juu ya vyote kabisa. Ikiwa hakuna ufufuko, wale wanaobatizwa kwa ajili ya wafu watafanya nini? Ikiwa wafu hawafufuki kabisa, kwa sababu gani watu wanabatizwa kwa ajili yao? Na sisi wenyewe, kwa nini tunahatarisha maisha yetu kila saa? Wandugu zangu, kila siku ninapatwa na hatari ya kufa. Na hii ni hakika sawa vile ninavyojivuna kwa ajili yenu katika kuungana kwangu na Yesu Kristo Bwana wetu. Ikiwa ni kwa nia ya kimutu, nimepigana na nyama wakali wa pori katika Efeso, jambo lile limenifalia nini? Kama wafu hawafufuki, basi: “Tukule na tukunywe, kwa maana kesho tutakufa.” Musidanganyike: “Warafiki wabaya wanaharibu tabia nzuri za watu.” Mugeuze mafikiri, murudie katika usawa, muache kufanya zambi. Ninasema neno hili kwa kuwapatisha haya, kwa sababu wamoja kati yenu hawamujui Mungu. Lakini labda kuko mutu anayeweza kuuliza: “Namna gani wafu watafufuka? Nao watakuwa na mwili wa namna gani wakati ule watakaporudia?” Wewe mujinga! Wakati unapopanda mbegu, mbegu ile haiwezi kuota isipokufa kwanza. Kile unachopanda si mumea muzima utakaopaswa kutokea nyuma, lakini ni punje tu, labda ya ngano au mbegu ingine fulani. Mungu anatokeza ndani ya ile punje umbo la mumea anaotaka; yeye anatokeza ndani ya kila mbegu umbo la kipekee. Miili ya viumbe vyote si sawa: watu wako na mwili wao wa kipekee, na nyama vilevile, na mwili wa ndege na samaki ni mbalimbali. Vilevile kuna miili ya mbinguni na miili ya dunia; nao uzuri wa miili ya mbinguni ni mbalimbali na uzuri wa miili ya dunia. Uzuri wa jua ni mbalimbali na uzuri wa mwezi, nao uzuri wa nyota ni mbalimbali, kwa maana hata nyota zinapishana uzuri vilevile. Itakuwa hivi vilevile wakati wafu watakapofufuka. Mwili unazikwa katika udongo katika hali ya kuharibika, lakini unapofufuka, unafufuka na hali ya kutoweza kuharibika na hali ya utukufu; nao unazikwa katika uzaifu, lakini unafufuka na nguvu. Wakati unapozikwa ni mwili wa kimutu, lakini unapofufuka unageuka mwili wa kiroho. Kama kuna mwili wa kimutu, basi kuna mwili wa kiroho vilevile. Kwa maana, Maandiko Matakatifu yanasema: “Mutu wa kwanza, Adamu, alikuwa kiumbe chenye uzima”; lakini Adamu wa mwisho ni Roho anayewapatia watu uzima. Si mwili wa kiroho unaotangulia lakini ni mwili wa kimutu, kisha ule wa kiroho unafuata. Adamu wa kwanza aliumbwa kwa udongo, yeye ni wa dunia, lakini Adamu wa pili alitoka mbinguni. Watu wa dunia wanafanana na yule aliyeumbwa kwa udongo, na watu wa mbinguni wanafanana na yule aliyetoka mbinguni. Na kama vile tulivyofanana na yule mutu aliyeumbwa kwa udongo, vilevile tutafanana na yule aliyetoka mbinguni. Wandugu zangu, muangalie, jambo ninalotaka kusema ni hili: kile kilichoumbwa kwa nyama na damu hakiwezi kupata urizi katika Ufalme wa Mungu katika hali ile, wala hakuna chenye hali ya kuharibika kinachoweza kuwa na hali ya kutoharibika. Sasa nitawaambia ninyi siri: sisi wote hatutakufa, lakini sisi wote tutabadilishwa kwa rafla, kama vile mutu anavyofunga jicho na kulifungua, wakati ngunga ya mwisho itakapolia. Kwa maana wakati itakapolia, wafu watafufuka na kupata kuwa katika hali ya kutoweza kufa tena, na sisi wote tutabadilishwa. Kwa maana sherti mwili huu wa kuharibika uvae mwili wa kutoharibika, na mwili wa kufa sherti uvae mwili wa kutokufa. Na wakati mwili huu wa kuharibika utakapovaa ule wa kutoharibika, nao mwili wa kufa utakapovaa ule wa kutokufa, halafu Maandiko Matakatifu haya yatatimia: “Kifo kimekomeshwa; kimeshindwa kabisa.” “Ewe kifo, ushindi wako uko wapi? Ewe kifo, uwezo wako wa kuua uko wapi?” Kifo kinapata uwezo wa kuua kutokana na zambi, na zambi inapata uwezo wake kutokana na Sheria. Lakini tumushukuru Mungu anayetupatia ushindi kwa njia ya Bwana wetu Yesu Kristo. Basi wandugu zangu wapenzi, musimame imara bila kutikisika. Muendelee kumutumikia Bwana siku zote, mukijua kwamba masumbuko munayopata kwa ajili ya Bwana hayatapita bure. Sasa juu ya muchango unaofanyika kwa ajili ya watu watakatifu wa Mungu wanaokuwa Yerusalema; ninyi vilevile mufanye sawa vile nilivyoagiza makanisa ya Galatia. Kila siku ya kwanza ya juma, kila mumoja wenu anapaswa kuweka akiba ya mali kwake, kwa kadiri ya mapato yake, kusudi musihitaji kufanya muchango wakati nitakapokuja. Nami nitakapofika, nitatuma watu mutakaochagua, pamoja na barua kwa kupeleka zawadi yenu Yerusalema. Ikiwa ni lazima mimi niende vilevile, basi nitasafiri pamoja nao. Nitakuja kwenu kisha kupitia Makedonia kufuatana na mupango wangu wa kupitia kule. Labda nitabakia pamoja nanyi muda kidogo, au tena wakati wote wa mvua kali; kusudi muweze kunisaidia kuendelea pahali popote nitakapokwenda. Kwa maana sitaki kuonana nanyi kwa kupita tu. Ninatumaini kukaa pamoja nanyi siku chache Bwana akitaka. Lakini, ninataka kubakia hapa Efeso, mpaka siku ya Pentekoste. Kwa maana nimepata hapa wakati muzuri wa kufanya kazi kubwa ijapokuwa wapinzani ni wengi. Kama Timoteo akifika, mujikaze kumupokea vizuri kati yenu kwa sababu yeye anafanya kazi ya Bwana kama mimi mwenyewe. Basi hata mutu mumoja asimuzarau. Lakini mumusaidie aendelee na safari yake katika amani; kusudi apate kurudia kwangu, maana ninamungojea yeye pamoja na wandugu waamini. Kwa ngambo ya ndugu yetu Apolo, nimemusihi sana akuje kwenu pamoja na wandugu wengine, lakini hakutaka kabisa kwenda sasa; atakwenda kwa wakati utakaomupendeza. Mukeshe, musimame imara katika imani, mukuwe hodari na wenye nguvu. Mutende mambo yenu yote katika upendo. Ninyi munajua Stefana na jamaa yake; munafahamu kwamba walikuwa watu wa kwanza walioamini katika inchi ya Akaya, nao wamejitoa kwa kutumikia watu wa Mungu. Hivi ninawasihi sana wandugu zangu, mukubali kuongozwa na watu kama hawa na wale wote wanaotumika na bidii pamoja nao. Nami ninafurahi kwa kufika kwa Stefana, Fortunato na Akaiko; wamekuwa kwa pahali penu, nao wamenifariji kama vile walivyowafariji ninyi wenyewe. Inafaa kuwakumbuka watu kama hawa. Makanisa ya jimbo la Azia yanawasalimia. Akila na Prisila pamoja na kanisa linalokusanyika ndani ya nyumba yao wanawasalimia sana katika Bwana. Wandugu wote wanaokuwa hapa wanawasalimia. Na ninyi vilevile musalimiane kwa upendo wa kikristo. Hii ni salamu ninayoiandika kwa mukono wangu mimi Paulo mwenyewe. Kama mutu hamupendi Bwana, alaaniwe! Bwana wetu, kuja! Neema ya Bwana Yesu ikuwe pamoja nanyi. Ninawapenda ninyi wote katika kuungana na Yesu Kristo. Barua hii inatoka kwangu mimi Paulo na kwa ndugu yetu Timoteo. Mimi ambaye kwa mapenzi ya Mungu, niliitwa kuwa mutume wa Kristo Yesu. Tunawaandikia kanisa la Mungu linalokuwa Korinto na watu wake wote wanaokuwa katika jimbo lote la Akaya. Tunawatakia neema na amani kutoka kwa Mungu Baba yetu na kwa Bwana Yesu Kristo. Asifiwe Mungu na Baba ya Bwana wetu Yesu Kristo, Baba mwenye kujaa huruma na Mungu anayefariji katika mambo yote! Yeye anatufariji katika taabu yetu yote, kusudi tupate kuwafariji wale wanaokuwa katika taabu yoyote kwa kuwaletea faraja tuliyopokea kutoka kwa Mungu. Basi, kwa kadiri tunavyoshiriki katika mateso mengi ya Kristo, ni kwa kadiri ile sisi vilevile tunafarijiwa sana kwa njia ya Kristo. Kama sisi tunapata taabu ni kusudi mupate kufarijiwa na kuokolewa. Kama tunafarijiwa ninyi vilevile munafarijiwa na kupata nguvu ya kuwawezesha kuvumilia taabu ile ile tunayopata. Kwa hivi, hatuwezi kukata tumaini tunalokuwa nalo kwenu, kwa maana tunajua kwamba kwa kuwa munashiriki katika taabu yetu, munashiriki vilevile katika kufarijiwa kwetu. Wandugu, tunataka mujue taabu tuliyopata katika jimbo la Azia. Taabu ile ilitulemea sana hata tukakata tumaini lote la kuendelea kuishi. Tulikuwa tumefikiri kwamba tulihukumiwa kufa. Basi, ilitokea hivi kusudi tusijitegemee sisi wenyewe, lakini tumutegemee Mungu tu anayefufua wafu. Yeye ndiye aliyetuopoa toka hatari kubwa sana ya kufa, naye atatuopoa tena. Nasi tunamutumainia kwamba ataendelea kutuopoa, nanyi wenyewe mutatusaidia kwa njia ya maombi. Kwa hivi Mungu atajibu kwa maombi yaliyotolewa na watu wengi kwa ajili yetu na kututendea wema, na watu wengi watamushukuru kwa ajili yetu. Jambo ambalo tunajivunia ni hili: zamiri yetu inayotuhakikishia kwamba tumeishi katika dunia na zaidi kati yenu katika uaminifu na ukweli tulivyojaliwa na Mungu. Sisi hatukuongozwa na hekima ya kimutu lakini na neema ya Mungu. Basi katika barua zetu tunawaandikia tu mambo yale munayoweza kusoma na kufahamu. Ninatumaini kwamba mutafahamu mambo haya kabisa, maana munayafahamu sasa kwa sehemu tu. Kwa Siku ile ya kurudi kwa Bwana wetu Yesu mutaweza kujivuna kwa ajili yetu kama vile tutakavyojivuna kwa ajili yenu. Katika tumaini hili nilikusudia kufika kwenu kwanza kusudi mupate furaha mara mbili. Nilikusudia kupitia kwenu kwa kwenda Makedonia, kisha ningewaona tena wakati wa kurudia, kwa hiyo mungenisaidia kwa safari yangu kwenda Yudea. Basi, nilipokusudia kubadilisha mupango wangu mimi nimekuwa kama kigeugeu? Wakati ninapofanya mipango yangu, mimi ninaongozwa na mafikiri ya kimutu hata nipate kusema “Ndiyo” na “Hapana” kwa mara moja? Kama vile Mungu anavyokuwa mwaminifu, hakika mambo tuliyowaambia hayakukuwa ya kusema “Ndiyo” na “Hapana” kwa mara moja. Kwa maana Yesu Kristo, Mwana wa Mungu ambaye Silvano, Timoteo na mimi mwenyewe tuliyemuhubiri kwenu hakukuja kusema “Ndiyo” na “Hapana.” Lakini yeye ni “Ndiyo” inayotoka kwa Mungu. Maana yeye ndiye anayetimiza ahadi zote za Mungu. Vilevile ni kwa njia ya Yesu Kristo tunasema “Amina” kwa kumutukuza Mungu. Ni Mungu mwenyewe ndiye anayetuimarisha pamoja nanyi katika ushirika na Kristo, na ni yeye mwenyewe ndiye aliyetuchagua. Ameweka kitambulisho juu yetu kinachohakikisha kama sisi ni watu wake na kuweka Roho Mutakatifu ndani yetu kuwa rehani ya vitu vyote anavyotuwekea. Ninamutaja Mungu kuwa mushuhuda wangu, yeye anajua roho yangu! Mimi nilikusudia kutorudia tena Korinto kwa sababu ya kuwasikilia huruma. Hatutafuti kuwaamuru ninyi juu ya mambo yale munayopaswa kuamini, maana munasimama imara katika imani. Lakini tunataka kutumika pamoja nanyi kusudi mupate kufurahi. Basi, nilikusudia kutorudia tena kwenu nikiwa mwenye huzuni. Kwa maana kama nikiwahuzunisha ninyi, ni nani atakayenifurahisha tena, isipokuwa tu wale niliowahuzunisha? Ni kwa sababu hii niliwaandikia kwamba sitakuja tena kwenu nisihuzunishwe na watu waliopaswa kunifurahisha. Maana nina uhakika kwamba mimi ninapofurahi, ninyi wote munafurahi vilevile. Niliwaandikia nikiwa mwenye kusikitika sana na mwenye kufazaika kabisa na nikilia machozi mengi, si kwa kuwahuzunisha ninyi, lakini ni kusudi mupate kujua namna gani ninavyowapenda. Kulikuwa mutu aliyefanya mambo ya kuhuzunisha, hakunihuzunisha mimi, lakini amewahuzunisha ninyi wote au bila kwenda mbali zaidi wamoja kati yenu. Azabu mutu yule aliyopewa na watu wengi kati yenu inatosha kwake. Basi sasa ni afazali kumusamehe na kumufariji, na kuepuka asikate kitumaini kwa sababu ya huzuni kubwa. Kwa hiyo ninawasihi ninyi kuhakikisha upendo wenu kwa mutu yule. Kwa maana shabaha yangu ya kuwaandikia ile barua ni kutaka kuwapima nipate kujua kwamba muko tayari kunitii siku zote. Wakati munaposamehe mutu, nami ninamusamehe vilevile. Kwa maana kama ninasamehe, na ikiwa kweli ninakuwa na neno lolote la kusamehe, ninasamehe mbele ya Kristo kwa ajili yenu, kusudi Shetani asipate njia ya kutushinda, maana tunajua nia zake. Wakati nilipofika katika muji Troa kwa kutangaza Habari Njema ya Kristo, Bwana alinipatia wakati muzuri wa kutumika kule. Ingawa vile, nilifazaika sana kwa sababu sikumukuta ndugu yangu Tito. Halafu nikaagana na watu wa muji ule na kwenda Makedonia. Lakini Mungu ashukuriwe, maana yeye ndiye anayetupatia ushindi siku zote katika ushirika wetu pamoja na Kristo. Anatutumia sisi kwa kutambulisha Kristo pahali pote kama vile harufu nzuri ya marasi inavyosambaa popote. Kwa maana sisi ni kama harufu nzuri iliyotolewa na Kristo kwa Mungu; na kunukia wale wanaookolewa na wale wanaopotea. Kwa wale wanaopotea ni harufu ya kifo inayoleta kifo; lakini kwa wale wanaookolewa, ni harufu ya uzima inayoleta uzima. Basi nani anayekuwa na uwezo wa kutimiza kazi ya namna hii? Basi sisi si kama wengine wengi wanaochuuza neno la Mungu; lakini kwa sababu Mungu ndiye aliyetutuma, sisi tunasema ukweli mbele yake, kama vile watumishi wa Kristo. Maneno haya yanaonyesha kwamba tunaanza kujisifu tena sisi wenyewe? Au tunahitaji kuwatolea ninyi barua za ushuhuda au kuziomba kwenu kama wengine? Ninyi wenyewe ni kama barua yetu ya ushuhuda iliyoandikwa katika mioyo yetu na watu wote wanaweza kuitambua na kuisoma. Inaonekana wazi kwamba ninyi ni barua iliyoandikwa na Kristo na kutumwa kwa njia ya utumishi wetu. Barua hii inaandikwa si kwa wino, lakini kwa Roho wa Mungu Mwenye Uzima. Barua hiyo haikuandikwa juu ya vibao vya mawe, lakini katika mioyo ya watu. Tunasema neno hili kwa ajili ya tumaini tunalokuwa nalo kwa Mungu kwa njia ya Kristo. Si kusema kwamba sisi wenyewe tuko na uwezo wa kujitungia jambo hili, lakini uwezo wetu unatoka kwa Mungu. Kwa maana Mungu ndiye aliyetuwezesha kuwa watumishi wa agano jipya, lisilotokana na Sheria iliyoandikwa, lakini na Roho. Sheria iliyoandikwa inaleta kifo lakini Roho analeta uzima. Sheria ile inayoleta kifo imeandikwa neno kwa neno juu ya vibao vya mawe na utukufu wa Mungu ulingaa wakati ule. Uso wa Musa ukangaa vilevile hata Waisraeli hawakuweza kuangalia uso wake ingawa kungaa kule kulikuwa kwa muda tu. Basi si zaidi sana matokeo ya utumishi wa Roho yatakuwa yenye utukufu? Ikiwa utumishi unaowaletea watu hukumu ulikuwa na utukufu, basi si zaidi sana utumishi unaowafanya watu wahesabiwe haki mbele ya Mungu, utakuwa na utukufu mukubwa zaidi? Tunaweza kusema kwamba ule utukufu uliongaa zamani hauwezi kulinganishwa na utukufu wa sasa unaokuwa mukubwa zaidi. Kwa maana kama mambo yaliyokuwa ya muda tu yalipata utukufu, basi yale yanayodumu ni yenye utukufu zaidi. Na kwa sababu tunakuwa na tumaini lile, sisi tunasema kwa uhodari. Sisi hatufanyi kama Musa alivyokuwa akifunika uso wake na kitambaa kwa kuzuiza Waisraeli wasiangalie mwisho wa utukufu uliokuwa wa muda tu. Lakini akili yao ilikuwa nzito kwa kufahamu. Kwa maana mpaka sasa, Waisraeli wanaposoma katika vitabu vya Agano la Kale, akili yao inafunikwa na kitambaa kile kile. Kitambaa kile kitaondolewa tu kwa mutu anayeungana na Kristo. Mpaka sasa, kila mara wanaposoma katika vitabu vya Musa, kitambaa kinafunika akili yao. Lakini “Wakati mutu anapomurudilia Bwana, kitambaa kile kinaondolewa.” Hapa “Bwana” ni Roho; na pahali Roho wa Bwana anapokaa, pale kuna uhuru. Sisi wote ambao uso haukufunikwa, tunaonyesha kama kioo utukufu wa Bwana. Kwa hiyo, tunabadilishwa kwa kufanana na Bwana, nasi tunapita toka utukufu mumoja hata utukufu mwingine unaokuwa mukubwa zaidi tena. Kwa maana kazi hii inatimizwa na Bwana ndiye Roho. Kwa wema wake, Mungu ametupatia utumishi huu, na kwa sababu hii sisi hatukati tumaini. Tumekataa mambo ya kisirisiri na ya haya. Hatuna mwenendo wa udanganyifu wala hatupotowi neno la Mungu. Lakini tunajulisha waziwazi ukweli kusudi tuvute kila mutu kutuaminia katika zamiri yake mbele ya Mungu. Lakini kama Habari Njema tunayotangaza ni ngumu kwa kusikia, ni kwa wale tu wanaofuata njia ya upotevu. Wao hawaamini kwa sababu yule mungu wa dunia hii amefunika akili zao. Yeye anawazuiza wasione mwangaza unaoletwa na Habari Njema ya utukufu wa Kristo, anayefanana na Mungu. Kwa maana, hatutangazi habari zetu sisi wenyewe, lakini tunatangaza kwamba Yesu Kristo ndiye Bwana, nasi tuko watumishi wenu kwa ajili ya Yesu. Yule Mungu aliyesema: “Mwangaza uangaze katika giza,” ndiye aliyeangaza ndani ya mioyo yetu, na kutuwezesha kufahamu utukufu wa Mungu unaongaa kwenye uso wa Kristo. Lakini sisi tunaokuwa na hazina hii ya kiroho, tuko vyombo vya udongo, kusudi watu waone waziwazi uwezo huu wa ajabu sana unaotoka kwa Mungu lakini si kwetu sisi wenyewe. Sisi tunagandamizwa kila namna, lakini hatushindwi; tunahangaishwa, lakini hatukati tumaini; tunateswa, lakini Mungu hatuachilii; tunatupwa chini, lakini hatuangamizwi. Kila wakati tunabeba mateso ya kufa kwa Yesu katika mwili wetu, kusudi uzima wa Yesu uonekane vilevile ndani ya mwili wetu. Kwa maana katika maisha yetu, tunakuwa kila mara katika hatari ya kufa kwa ajili ya Yesu, kusudi uzima wake uonekane vilevile katika mwili wetu unaokuwa wa kufa. Kwa hivi, kifo kinafanya kazi ndani yetu, lakini uzima unafanya kazi ndani yenu. Maandiko Matakatifu yanasema: “Niliamini ndiyo maana nilisema.” Sisi vilevile tunakuwa na imani ile ile, ndiyo maana tunasema. Tunajua kwamba Mungu aliyemufufua Bwana Yesu atatufufua sisi vilevile pamoja na Yesu. Yeye atatufikisha pamoja nanyi mbele ya Yesu. Kwa maana mambo haya yote yanafika kwa ajili yenu kusudi neema ya Mungu izidishwe kwa watu wengi siku zote, nao wapate kumutolea Mungu shukrani nyingi kwa ajili ya utukufu wake. Kwa sababu hii hatukati tumaini hata kidogo. Ijapokuwa hali yetu ya kimwili inaharibika, hali yetu ya kiroho inafanywa upya siku kwa siku. Kwa maana taabu tunayopata ni ndogo na ya muda tu, inatutayarishia utukufu mukubwa sana na wa milele unaokuwa muzuri zaidi kupita mateso haya. Maana sisi hatuangalii vitu vile vinavyoonekana, lakini vitu visivyoonekana. Kwa sababu vile vinavyoonekana vinadumu muda kidogo tu, lakini vile visivyoonekana, vinadumu milele. Kwa maana, tunajua kwamba hema hii tunayoishi ndani yake hapa katika dunia, maana yake mwili wetu, itakapobomolewa, Mungu atatupatia makao mengine mbinguni. Nayo ni nyumba aliyoijenga yeye mwenyewe na inayodumu milele. Na sasa katika hali hii tunaugua kwa maana tunatamani sana kuvaa makao yetu yanayotoka mbinguni. Kwa maana, tukisha kuyavaa hatutaonekana tena kuwa uchi. Hakika kwa wakati wowote tungali tunaishi katika makao haya ya dunia, tunaugua kwa kulemewa. Si kwa sababu tunataka kuondolewa mwili wa dunia, lakini tunataka kuvaa mwili wa mbinguni, kusudi uzima wa milele upate kubadilisha miili yetu inayokuwa ya kufa. Ni Mungu mwenyewe aliyetuwezesha kupata mabadiliko hayo na kuweka Roho Mutakatifu ndani yetu kuwa rehani ya vitu vyote anavyotuwekea. Basi tuna uhodari siku zote. Tunajua kwamba wakati tunapoishi katika mwili huu, tunaishi mbali na makao ya Bwana. Kwa maana tunaishi kwa imani lakini si kwa kuona. Sisi tuna uhodari na tungependa zaidi kutoka katika mwili huu na kwenda kuishi pamoja na Bwana. Lakini mbele ya yote tunataka sana kumupendeza Bwana, ikiwa tunakaa au kutoka katika mwili huu. Kwa maana sisi wote tunapaswa kusimama kwa kusambishwa mbele ya tribinali ya Kristo, kusudi kila mutu alipwe kufuatana na matendo yake mema au mabaya aliyofanya alipokuwa akiishi ndani ya mwili wake. Basi, kwa sababu tunajua kwamba ni lazima kumwogopa Bwana, ndiyo maana tunajitoa kuwavuta watu kwake. Mungu anatujua waziwazi nami ninatumaini kwamba ninyi wenyewe munatujua waziwazi vilevile. Sisi hatuanzi tena kujisifu wenyewe mbele yenu, lakini tunawapa ninyi sababu ya kuweza kujivuna kwa ajili yetu. Hivi tena munaweza kupata maneno ya kuwajibu wale wanaojivunia tu hali yao ya inje, lakini si mambo yanayokuwa ndani ya mioyo yao. Ikiwa kweli tunaonekana kuwa wenda-wazimu, ni kwa ajili ya Mungu, lakini kama sisi ni wenye akili sawa, ni kwa faida yenu. Maana upendo wa Kristo unatuongoza sisi tunaokubali kwamba ni mutu mumoja tu ndiye aliyekufa kwa ajili ya watu wote; maana yake wote wanashiriki katika kifo chake. Naye alikufa kwa ajili ya watu wote, kusudi wale wanaoishi, wasiishi kwa ajili yao wenyewe, lakini kwa ajili ya yule aliyekufa na kufufuka kwa ajili yao. Kwa hiyo basi, tangu sasa hatumuhesabu tena mutu yeyote kufuatana na hali ya kimutu. Hata ikiwa tulimuhesabu Kristo kufuatana na hali ya kimutu, kwa sasa hatumuhesabu tena kufuatana na hali ile. Basi mutu yeyote anapoungana na Kristo, yeye anakuwa kiumbe kipya. Mambo ya zamani yametoweka, na sasa hali mupya imefika. Mambo haya yote yalifanyika na Mungu, aliyetupatanisha naye kwa njia ya Kristo na kutupatia kazi ya kuongoza watu wengine wapatane naye. Ndiyo kusema, Mungu ndiye aliyekuwa akipatanisha watu wote na yeye mwenyewe kwa njia ya Kristo bila kuhesabu makosa yao. Yeye ametupatia ujumbe wa upatanisho. Basi sisi ni wajumbe wa Kristo. Kwa njia yetu, Mungu mwenyewe anawaita ninyi; na kwa hiyo tunawasihi katika jina la Kristo, mukubali kupatanishwa na Mungu. Kwa maana Kristo alikuwa bila zambi, lakini Mungu alimubebesha muzigo wa zambi zetu, kusudi kwa njia yake tupate kuwa wenye haki mbele ya Mungu. Basi, sisi tunaotumika pamoja na Mungu, tunawasihi musipoteze bure neema muliyopokea kwake. Kwa maana Mungu anasema hivi katika Maandiko Matakatifu: “Kwa wakati uliofaa, nilijibu maombi yako. Kwa siku ya wokovu, nilikusaidia.” Basi sasa, huu ndio wakati unaofaa, sasa leo ni siku ya wokovu. Sisi hatutaki kumukwaza mutu yeyote katika jambo lolote kusudi kazi yetu isizarauliwe. Lakini tunaonyesha katika mambo yote kwamba sisi ni watumishi wa Mungu: tumedumu sana katika mateso, katika ukosefu na katika taabu. Tumepigwa, tumetiwa ndani ya kifungo, wamefanya fujo juu yetu, tumefanya kazi ngumu, tumekoseshwa usingizi na kukaa bila kula. Tunaonyesha kwamba sisi ni watumishi wa Mungu kwa njia ya usafi wa moyo wetu, ya ufahamu, ya uvumilivu, ya wema wetu, ya Roho Mutakatifu, ya upendo wetu wa kweli, ya ujumbe wa neno la kweli, na ya uwezo wa Mungu. Tunatumia kama vile silaha mambo ya haki kwa kushambulia na kujikinga. Tunaheshimiwa na kuzarauliwa, tunatukanwa na kusifiwa. Tunahesabiwa kama wenye kusema uongo, ingawa sisi tunasema ukweli, kama watu wasiojulikana ingawa tunajulikana vizuri, kama wanaokufa ingawa sisi ni wazima. Tunaazibiwa lakini hatuuawi, tunahuzunishwa lakini tunafurahi siku zote. Tunaonekana kama wamasikini lakini tunatajirisha watu wengi, hatuna kitu, lakini tunakuwa na vitu vyote. Ee ninyi Wakorinto! Tumesema nanyi waziwazi na tumewafungulia kabisa moyo wetu. Sisi hatukuwafungia mioyo yetu, lakini ni ninyi ndio muliotufungia moyo wenu. Sasa ninasema nanyi kama vile watoto wangu: kwa ngambo yenu mutufungulie nasi moyo wenu vilevile. Musishirikiane pamoja na watu wasioamini. Kwa maana kuna ushirika gani kati ya haki na uovu? Kuna mapatano gani kati ya mwangaza na giza? Kuna masikilizano gani kati ya Kristo na Shetani? Au mutu anayeamini yuko na ushirika gani na mutu asiyeamini? Kuna ulinganisho gani kati ya hekalu la Mungu na sanamu? Kwa maana sisi ni hekalu la Mungu Mwenye Uzima kama vile yeye mwenyewe alivyosema: “Nitakaa na kuishi pamoja nao, nitakuwa Mungu wao, nao watakuwa watu wangu.” Kwa sababu hiyo Bwana anasema: “Mutoke kati yao, mujitenge nao. Musiguse kitu chochote kinachohesabiwa kuwa kichafu, nami nitawapokea. Nitakuwa Baba yenu nanyi mutakuwa wana na wabinti wangu. Ni mimi Bwana Mwenye Uwezo ninayesema.” Basi wapendwa wangu, kwa kuwa tumepewa ahadi hizi zote, tujitakase toka uchafu wote unaochafua mwili na roho na tujikaze kuwa watakatifu kabisa tukiishi katika kumuheshimu Mungu. Mutufungulie moyo wenu! Hatukumukosea mutu yeyote, hatukumunyanganya mutu yeyote, wala kumupotosha mutu yeyote. Sisemi vile kwa kuwahukumu. Kwa maana, kama vile nilivyokwisha kusema, ninyi ni wapendwa wetu, ikiwa katika kuishi au katika kufa. Mimi ninawaaminia sana na kujivuna kwa ajili yenu. Katika mateso yetu yote, ninafarijiwa sana na kujazwa na furaha. Kwa maana hata wakati tulipofika Makedonia, hatukuweza kupumzika hata kidogo. Tulipata taabu pande zote: magomvi pamoja na watu wengine, na woga katika moyo wetu. Lakini Mungu anayefariji watu wanyenyekevu, ametufariji kwa njia ya kufika kwa Tito. Nasi hatukufarijiwa kwa kuja kwake tu, lakini vilevile kwa namna ile mulivyomufariji. Tito ametuelezea jinsi munavyokuwa na hamu kubwa ya kuniona, jinsi munavyohuzunika na jinsi munavyojitoa kwa ajili yangu. Kwa hivi sasa ninafurahi zaidi. Basi, ikiwa nimewahuzunisha na barua yangu, sijuti juu yake sasa. Nilijuta wakati nilipotambua kwamba barua ile iliwahuzunisha ingawa ilikuwa ni kwa muda tu. Sasa ninafurahi, si kwa sababu muliweza kuhuzunika, lakini kwa sababu huzuni yenu imewawezesha kugeuka toka katika zambi. Kwa maana mumehuzunishwa kufuatana na mupango wa Mungu. Kwa hivi hatukuwatendea ubaya wowote. Basi, huzuni inayosababishwa na Mungu inamuwezesha mutu kugeuka toka katika zambi. Na kugeuka kule, kunamuletea kuokoka. Kule kuokoka hakuleti majuto. Lakini huzuni inayosababishwa na mwanadamu inaleta kifo. Basi, muangalie sasa matokeo ya ile huzuni inayosababishwa na Mungu! Imewafanya kuwa wenye bidii sana, wenye kujitetea, wenye kuonyesha kwamba hamuna kosa, wenye utii, wenye hamu kubwa ya kuniona, wenye kujitoa kwa ajili yangu na wenye kutaka kabisa kuazibu ubaya. Mumeonyesha katika njia zote kwamba hamukukuwa na kosa katika mambo haya. Basi ikiwa nimewaandikia, si kwa ajili ya yule aliyefanya kosa au si kwa ajili ya yule aliyemukosea. Lakini kusudi mupate kutambua waziwazi mbele ya Mungu bidii munayokuwa nayo kwa ajili yetu. Hii ndiyo maana tumefarijiwa. Lakini zaidi ya kufarijiwa kwetu tulifurahi tena sana kwa ajili ya furaha Tito aliyokuwa nayo kufuatana na jinsi mulivyomutuliza. Mimi nimejivuna kidogo mbele yake kwa ajili yenu, nami sikupata haya. Lakini kama vile tulikuwa tunawaambia kila mara ukweli, vilevile kule kujisifu kwetu kwa ajili yenu mbele ya Tito, kumeonekana kuwa kwa kweli. Mapendo yake kwa ajili yenu yanazidi kuongezeka anapokumbuka vile mulivyokuwa tayari kumutii na vile mulivyomupokea kwa woga na kutetemeka. Ninafurahi sana kwa sababu ninaweza kuwaaminia katika kila jambo. Wandugu, tunapenda kuwajulisha namna Mungu alivyojalia neema makanisa ya Makedonia. Yalijaribiwa sana kwa njia ya mateso mengi yaliyopata. Lakini yalizidi kuwa na furaha hata yakakuwa na moyo wa kutoa kupita kipimo, ingawa yalikuwa masikini sana. Ninayashuhudia kwamba kwa mapenzi yao yalitoa kwa kadiri yalivyoweza na hata zaidi kupita uwezo wao. Yalitusihi sana tukishiriki nayo katika kazi ya kuwasaidia watu wa Mungu wanaokaa Yudea. Yalitoa kupita vile tulivyokuwa tukitumaini! Kwanza yalijitoa yenyewe kwa ajili ya kazi ya Bwana, kisha yakajitoa kwa ajili yetu vilevile kufuatana na mapenzi ya Mungu. Ni kwa hiyo tulimusihi Tito atimize kazi hiyo ya kuwaongoza ninyi kuwa na moyo wa kutoa sawa alivyoianzisha. Ninyi munakuwa na kila kitu kwa uwingi: imani, usemi, ufahamu, kuwa na bidii ya kila namna na upendo munaokuwa nao kwetu. Kufuatana na hiyo mukuwe vilevile na uwingi katika kazi hii ya kuwa na moyo wa kutoa. Sisemi hivi kwa kuwaamuru, lakini kwa njia ya kuwaelezea habari za bidii ya wengine, ninataka kuwapima kusudi upendo wenu upate kutambulikana kuwa wa kweli. Kwa maana munajua neema ya Bwana wetu Yesu Kristo, ingawa alikuwa tajiri, yeye mwenyewe alijifanya masikini kwa ajili yenu, kusudi mupate kuwa watajiri kwa njia ya umasikini wake. Kuelekea jambo hilo, mimi ninawatolea shauri, nalo linafaa kwenu, kwa maana ni ninyi muliokuwa wa kwanza kukusudia kufanya kazi ile na kuianzisha tangu mwaka jana. Sasa muendelee nayo na kuitimiza. Kama vile mulivyokuwa na moyo mwema wa kukusudia kuifanya, basi mukuwe na moyo mwema wa kuitimiza kufuatana na uwezo wa mali munayokuwa nayo. Kwa maana kama mutu akiwa na moyo wa kutoa, Mungu anakubali kitu anachotoa kufuatana na kile anachokuwa nacho, wala si kufuatana na kile asichokuwa nacho. Nia yangu si kusema kwamba munapaswa kujitia katika taabu kwa ajili ya kusaidia watu wengine, lakini inafaa kuwe usawa. Na sasa ninyi muko na mapato mengi zaidi, basi munaweza kuwasaidia wale wanaokuwa katika mahitaji. Hivi wao vilevile watakapokuwa na mapato mengi wataweza kuwasaidia katika siku za mahitaji. Kwa hiyo kutakuwa usawa kama vile Maandiko Matakatifu yanavyosema: “Yule aliyeokota kingi hakukuwa na cha zaidi, na aliyeokota kidogo, hakupungukiwa.” Shukrani kwa Mungu aliyemutia Tito bidii ya kuwasaidia kama vile sisi tunavyokuwa nayo! Amekubali ombi letu, na zaidi ya ile ameondoka kuja huko kwenu kwa bidii yake kubwa na kutokana na mapenzi yake mwenyewe. Pamoja naye tunamutuma ndugu anayesifiwa na makanisa yote kwa ajili ya kazi yake ya kuhubiri Habari Njema. Vilevile, yule ndugu amechaguliwa na makanisa kwa kutusindikiza katika safari ya kutimiza kazi hii ya kutoa kwa moyo mwema ambayo sisi tunafanya kwa ajili ya utukufu wa Bwana, na kwa kuonyesha nia yetu ya kusaidia watu wengine. Tunaepuka kushitakiwa na watu wengine juu ya mali mingi kama hii tunayochunga. Kwa maana tunataka kufanya mema, si mbele ya Bwana tu, lakini mbele ya watu vilevile. Tunatuma ndugu yetu mwingine pamoja nao. Sisi tumemupima mara nyingi na ameonyesha siku zote kwamba yeye ni mwenye bidii sana. Na sasa, yeye ni mwenye bidii zaidi tena kwa kuwa anawaaminia ninyi sana. Kwa ngambo ya Tito, yeye ni mwenzangu, ninafanya kazi pamoja naye kwa ajili yenu. Nao wale wandugu wengine wanaomusindikiza, ni wajumbe wa makanisa wanaotumika kwa ajili ya utukufu wa Kristo. Kwa hiyo muonyeshe mbele ya makanisa kwamba hakika munawapenda na kuyafahamisha kwamba tulikuwa na haki ya kujivuna kwa ajili yenu. Si lazima niwaandikie juu ya musaada unaotumwa kwa watu wa Mungu wanaokuwa katika Yudea. Kwa maana ninajua nia yenu nzuri ya kusaidia, nami ninajivuna kwa ajili yenu mbele ya watu wa Makedonia, nikisema: “Kanisa la jimbo la Akaya liko tayari kusaidia tangia mwaka jana.” Hivi kwa njia ya bidii yenu mumewavuta wengi kati yao kwa kutoa vilevile. Lakini sasa ninawatumia wandugu hawa kusudi kujisifu kwetu kwa ajili yenu kusionekane kuwa bure. Kwa hiyo ninataka mukuwe tayari kama vile nilivyosema. Kwa maana kama watu wa Makedonia wanakuja pamoja nami na tusipowakuta tayari, sisi tutapata haya sana kwa kuona jinsi nilivyowaaminia, nami sisemi kitu juu ya haya ambayo ninyi mutaweza kupata. Ni hivi niliona kuwa ni vizuri kuwashauri wandugu hawa watangulie kufika kwenu mbele yangu kusudi watayarishe vile vitu mulivyoahidi kutoa kwa mapenzi yenu. Hivi vitakuwa tayari na itaonyesha kwamba mumevitoa kwa moyo mwema, wala si kwa uchoyo. Mukumbuke maneno haya: yule anayepanda kidogo atavuna kidogo, na yule anayepanda kwa uwingi atavuna kwa uwingi. Basi inafaa kila mutu atoe sawa alivyokusudia, si kwa huzuni wala si kwa kulazimishwa. Kwa maana Mungu anapenda mutu yule anayetoa kwa furaha. Na Mungu anaweza kuwajalia mema ya kila namna, kusudi siku zote mupate vyote munavyohitaji, na hivi mupate kuzidi kutoshelewa katika kutenda kazi njema. Kama vile inavyoandikwa katika Maandiko Matakatifu: “Ametoa kwa uwingi, amewapa wamasikini. Haki yake inadumu milele.” Mungu ndiye anayemupatia mupandaji mbegu na mukate wa kukula. Kwa hiyo atawapatia ninyi mbegu yoyote munayohitaji na kuiotesha, kusudi moyo wenu wa kutoa upate kuzaa matunda mengi. Hivi mutakuwa watajiri katika vitu vyote, kusudi siku zote muweze kuonyesha moyo wa kutoa, hata watu wengi watamushukuru Mungu kwa ajili ya musaada tunaowafikishia kutoka kwenu. Kwa maana kazi hii ya kutoa munayofanya haifai tu kwa kusaidia watu wa Mungu kusudi wapate vitu wanavyokosa, lakini vilevile kwa njia ile watu wengi wanamutolea Mungu shukrani. Kufuatana na ushuhuda wa kazi hii, watu watamutukuza Mungu kwa kuona jinsi munavyoonyesha utii wenu katika kushika Habari Njema ya Kristo. Vilevile wanamutukuza kwa kuona moyo wa kutoa munaokuwa nao katika kushirikiana mali yenu pamoja nao na sisi. Kwa hiyo watawaombea kwa upendo mwingi, kwa ajili ya neema kubwa sana Mungu aliyowajalia. Shukrani kwa Mungu kwa ajili ya zawadi yake inayopita kipimo! Sasa mimi Paulo mwenyewe ninawaomba kwa upole na kwa wema sawa na ule wa Kristo; mimi yule ambaye wanasema juu yake kwamba ni mupole wakati ninapokuwa pamoja nanyi, lakini ni mukali wakati ninapokuwa mbali nanyi. Ninawasihi kwamba nitakapofika kwenu, musinisukume kuwa mukali. Kwa maana nina uhakika kwamba nitawatendea vile wale watu wote wanaozania kwamba sisi tunaishi maisha ya kimwili. Kwa maana ijapokuwa tunaishi katika dunia, lakini hatufanyi vita kwa namna ya kimwili. Silaha tunazotumia katika vita si za kimwili, lakini silaha zetu ni uwezo wa Mungu unaoweza kuharibu upango wa adui. Tunaharibu mawazo ya uongo na kuangusha vizuizo vyote watu wanavyojivunia kwa kupinga elimu ya Mungu. Tunatawala mafikiri ya watu na kuyafanya yapate kumutii Kristo. Sisi tuko tayari kuazibu kila kitendo cha uasi, mutakapoonyesha kwamba munatii kabisa. Ninyi munaangalia tu namna vitu vinavyoonekana kwa inje. Mutu yeyote anayejiaminia kwamba yeye ni wa Kristo, inafaa afikiri tena yeye mwenyewe mambo haya: ikiwa yeye ni wa Kristo sisi vilevile ni wa Kristo. Kwa maana sioni haya hata kama nimejivuna zaidi kwa ajili ya uwezo Bwana aliotupatia sisi. Kwa maana uwezo ule ni kwa ajili ya kuwajenga katika imani, lakini si wa kubomoa. Sitaki kuonekana kwamba ninataka kuwaogopesha kwa barua zangu. Kwa sababu wengi wanasema: “Barua za Paulo ni kali na zenye maneno mazito; lakini yeye mwenyewe anapokuwa katikati yetu ni muzaifu na namna yake ya kusema ni ya kuzarauliwa.” Inafaa mutu yule anayesema vile ajue vema kwamba hakuna tofauti kati ya maneno tunayoandika katika barua zetu wakati tunapokuwa mbali, na yale tutakayofanya wakati tutakapokuwa pamoja nanyi. Kwa kweli hatungesubutu kujifananisha au kujilinganisha na watu wale wanaojisifu wenyewe. Wao ni wapumbafu. Wanajipima kufuatana na kipimo chao wenyewe na kujilinganisha na wao wenyewe. Sisi hatutajivuna kupita kipimo, lakini tunataka kutumia kile kipimo cha kazi ile Mungu aliyotupatia na iliyotufikisha vilevile mpaka kwenu. Hatutambuki mipaka yetu sawa vile hatukufika kwenu. Kwa maana tulifika kwenu, tukiwatangazia Habari Njema ya Kristo. Basi, hatujivuni kupita kipimo juu ya kazi ya watu wengine. Lakini tunatumaini kwamba imani yenu itakapokuwa ikiongezeka, tutaweza kufanya kazi kubwa zaidi kati yenu kufuatana na kipimo cha kazi tuliyopewa na Mungu. Kisha tutaweza kuhubiri Habari Njema katika inchi zinazokuwa mbali kupita inchi yenu, kuliko kujisifu juu ya kazi watu wengine waliyokwisha kufanya kufuatana na kipimo walichopewa. Lakini, kama Maandiko Matakatifu yanavyosema: “Anayetaka kujivuna, ajivune kwa ajili ya Bwana.” Kwa maana, mutu anayekubaliwa si yule anayejisifu mwenyewe, lakini ni yule anayesifiwa na Bwana. Ingekuwa heri muvumilie kidogo masemi yangu ya upumbafu! Ninawaomba kweli munivumilie! Mimi ninasikia wivu kwa ajili yenu sawa vile Mungu anavyousikia vilevile. Kwa maana ninyi ni kama binti mukamilifu niliyemwowesha kwa mume mumoja, ndiye Kristo. Lakini ninaogopa kwamba sawa vile nyoka alivyomudanganya Eva kwa werevu wake, mawazo yenu vilevile yasipotoshwe hata mupate kupoteza uaminifu na ukamilifu wenu kwa Kristo. Hii inatokana na kuona jinsi munavyomukubali mutu yeyote anayekuja kwenu na kuwahubiri habari za Yesu mwingine asiyekuwa yule sisi tuliyemuhubiri. Na zaidi ya hii munakubali upesi kupokea roho ingine na ujumbe mwingine vinavyokuwa tofauti na Roho au Habari Njema muliyopokea toka kwetu. Ninazani kwamba wale mitume wanaohesabiwa kuwa wakubwa zaidi hawanipiti kitu kabisa. Inaonekana kuwa mimi si mutu anayeelewa kusema, lakini kwa ngambo ya elimu, mimi ninaielewa sana. Nasi tumeonyesha hayo yote kila wakati na katika mambo yote. Mimi niliwatangazia Habari Njema ya Mungu bila kudai mushahara. Nilijinyenyekeza kusudi mupate kutukuzwa. Basi kwa kujinyenyekeza vile, nilifanya kosa? Nilipokuwa nikitumika kati yenu nililipwa na makanisa mengine. Ni kama vile nilinyanganya mali ya makanisa yale na kuitumia kwa kuwasaidia. Wakati nilipokuwa kwenu, sikumulemea mutu yeyote nilipohitaji kitu fulani, kwa maana wandugu waliotoka Makedonia waliniletea vitu vyote nilivyohitaji. Nilijiangalia vizuri katika mambo yote kusudi nisiwalemee, nami nitaendelea kujiangalia vema. Kufuatana na vile ninavyosema ukweli kama vile Kristo, ninaapa kwamba hakuna anayeweza kunizuiza kujivuna juu ya jambo hilo katika jimbo lote la Akaya. Kwa sababu gani ninasema hivi? Kwa sababu siwapendi? Hapana, Mungu anajua kwamba ninawapenda. Nitaendelea kufanya sawasawa ninavyofanya kwa sasa, kusudi niwafungie njia zote wale wanaotafuta kujivuna kwamba wanatumika sawa sisi. Watu wale ni mitume wa uongo, wanafanya kazi yao kwa udanganyifu wakijisingizia kuwa mitume wa kweli wa Kristo. Na jambo hilo si la kushangaza kwa maana Shetani mwenyewe anajisingizia kuwa malaika wa mwangaza. Basi si jambo la ajabu kama watumishi wake vilevile wanajigeuza kuwa watumishi wa haki. Kwa mwisho wao watalipwa kufuatana na matendo yao. Mimi ninasema tena: mutu asinizanie kuwa mupumbafu. Kama si vile, basi munihesabu kama mupumbafu, kusudi nami nipate kujivuna kidogo vilevile. Maneno haya ninayosema sasa hayafuatani na mapenzi ya Bwana, lakini ninayasema tu kama mupumbafu kuelekea jambo hili la kujivuna. Watu wengi wanajivuna kwa namna ya kimwili, kwa sababu hiyo mimi nitajivuna vilevile. Ninyi munajidai kuwa wenye hekima na ndiyo maana munapenda kuwavumilia wapumbafu! Munavumilia hata mutu anayewatia katika utumwa, anayeiba mali zenu, anayewagandamiza, anayewazarau na anayewapiga kofi kwenye uso. Ninasikia haya ya kuisema: tumekuwa zaifu kwa kufanya vile! Lakini kama watu wengine wanasubutu kujivuna juu ya kitu chochote, mimi vilevile nitajivuna. Sasa ninasema kama vile mupumbafu. Watu wale ni Waebrania? Mimi vilevile. Wao ni Waisraeli? Mimi vilevile. Wao ni wa uzao wa Abrahamu? Mimi vilevile. Sasa nitasema kama mwenda-wazimu: wao ni watumishi wa Kristo? Mimi ni mutumishi wake zaidi kuliko wao. Nimetumika kazi nyingi zaidi, nimefungwa mara nyingi zaidi, nimepigwa zaidi, na mara nyingi nimekuwa katika hatari ya kufa. Mara tano Wayuda wamenipiga viboko makumi tatu na tisa. Waroma wamenipiga fimbo mara tatu na mara moja walitaka kuniua kwa kunitupia mawe. Mara tatu chombo nilichosafiri nacho kilizama kwa kuvunjika. Mara moja, nilishinda ndani ya bahari kwa muda wa siku nzima. Katika safari zangu nyingi nimepata hatari ya mafuriko ya mito, hatari ya wanyanganyi, hatari kutoka kwa wanainchi wenzangu na kutoka kwa watu wa mataifa mengine. Nilikuwa katika hatari ndani ya miji, katika jangwa, katika bahari na kati ya wandugu za uongo. Nimesumbuka kwa kufanya kazi ngumu, nimepata magumu, nimekesha mara nyingi. Mara nyingi niliteswa na njaa na kiu; mara nyingi nililazimishwa kutokula. Nimeteseka na baridi na ukosefu wa nguo. Na bila kutaja mambo yote mengine kama hayo, kila siku ninashugulika na makanisa yote. Kukiwa mutu anayepatwa na uzaifu, mimi ninajisikia muzaifu vilevile. Kukiwa mutu anayeanguka katika zambi, ninasikia uchungu. Kama ikinipasa kujivuna nitajivuna kwa ajili ya uzaifu wangu. Mungu Baba ya Bwana Yesu, anayetukuzwa hata milele, anajua kwamba sisemi uongo. Wakati nilipokuwa Damasiki, liwali wa mufalme Areta aliweka walinzi katika muji ule kusudi wanikamate. Lakini wakanitia ndani ya kitunga na kunishusha kwenye ukuta wa muji, tokea ndani ya dirisha, nami nikapata kuponyoka. Basi nitaendelea kujivuna ijapokuwa si vizuri. Lakini nitasema sasa juu ya maono na ufunuo nilivyopata toka kwa Bwana. Ninamujua mutu mumoja aliyeungana na Kristo, na sasa kumekwisha kupita miaka kumi na mine, mutu huyu akanyanyuliwa mpaka katika mbingu ya tatu. (Ikiwa alinyanyuliwa katika hali ya kimwili au ya kiroho mimi sijui, Mungu peke yake anajua.) Nami ninajua kwamba mutu yule alinyanyuliwa mpaka katika Paradizo. (Ninasema tena ikiwa mutu yule alinyanyuliwa katika hali ya kimwili au ya kiroho mimi sijui, Mungu peke yake anajua.) Katika Paradizo, mutu yule akasikia mambo ya ajabu na yasiyoruhusiwa kwa mwanadamu kuyaeleza. Basi, nitajivuna kwa ajili ya mutu sawa na yule, lakini sitajivuna kwa ajili yangu mimi mwenyewe, isipokuwa tu kwa ajili ya uzaifu wangu. Kama ningetaka kujivuna, singekuwa mupumbafu, maana ningesema tu ukweli. Lakini ninaepuka kujivuna, kusudi watu wasinihesabu kuwa mukubwa kuliko vile wanavyoona nikifanya au kunisikia nikisema. Lakini, kusudi nisijivune kupita kipimo kwa ajili ya kupokea ufunuo wa ajabu, nilitiwa katika mwili wangu kitu kinachoniumiza kama mwiba. Kitu kile ni kama mujumbe wa Shetani kwa kunipiga na kunizuiza nisijivune kupita kipimo. Nami nilimusihi Bwana mara tatu kusudi aniondolee kitu kile. Lakini akanijibu: “Neema yangu inakutoshelea, kwa maana uwezo wangu unatimizwa katika uzaifu.” Basi tafazali nijivunie sana uzaifu wangu kusudi nijazwe na uwezo wa Kristo. Kwa sababu hii ninafurahia uzaifu, matusi, ukosefu, taabu na mateso kwa ajili ya Kristo. Kwa maana wakati ninapokuwa muzaifu, basi ndio wakati ule ninapokuwa na nguvu. Ninasema kama mupumbafu, lakini ni ninyi ndio mumenilazimisha kufanya vile. Kufuatana na ile, ningepaswa kusifiwa nanyi. Kwa maana hata kama mimi si kitu, wale mitume wenu wanaohesabiwa kuwa wakubwa hawanipiti kitu kabisa. Matendo yanayohakikisha kwamba mimi ni mutume yamefanyika kati yenu kwa uvumilivu wote, kwa njia ya miujiza, maajabu, na vitambulisho. Mumepungukiwa na nini kuliko makanisa mengine, isipokuwa tu kwamba mimi sikuwalemea kwa kupata musaada toka kwenu? Munisamehe kwa kosa hili. Sasa mimi niko tayari kufika kwenu kwa mara ya tatu, nami sitawalemea. Maana sihitaji mali yenu, lakini ninawahitaji ninyi. Kwa sababu si kazi ya watoto kuwawekea wazazi wao akiba, lakini ni kazi ya wazazi kuwawekea watoto wao akiba. Kwa ngambo yangu, nitafurahi kutumia vyote ninavyokuwa navyo na kujitoa mimi mwenyewe, kwa ajili yenu. Ikiwa ninawapenda zaidi namna hii, hamupaswi kupungukiwa na upendo kwangu. Basi mutakubali kwamba mimi sikuwalemea. Lakini watu wengine wanafikiri kwamba mimi ni mwerevu na nimewanasa kwa kuwadanganya. Basi niliwaibia ninyi kwa njia ya mutu mumoja kati ya wale niliowatuma kwenu? Nilimusihi Tito aende kwenu na nimemutuma pamoja na ndugu mwingine. Munaweza kusema kwamba Tito amewaibia ninyi? Basi mimi pamoja naye tuliishi katika nia moja na kuwa na mwenendo mumoja. Ninyi munazani kwamba kwa wakati huu wote sisi tunajitetea mbele yenu? Tunasema mambo yale mbele ya Mungu kufuatana na vile tunavyoungana na Kristo. Wandugu wapendwa, mambo yale yote ni kwa kuwajenga ninyi katika imani. Kwa maana ninaogopa kwamba wakati ninapokuja kwenu, sitawakuta sawa vile ninavyotaka, nanyi hamutanikuta sawa vile munavyotaka. Ninaogopa kuwakuta katika fitina, wivu, kasirani, ugomvi, masingiziano, matetano, majivuno na fujo. Ninaogopa kwamba kwa safari yangu ingine, Mungu wangu atanifanya tena kuwa mwenye haya mbele yenu. Nami nitalia kwa ajili ya watu wengi waliofanya zambi zamani nao hawakugeuka toka katika uasherati, uzinzi na tamaa mbaya walizofanya. Hii ni safari yangu ya tatu ninayotayarisha kuja kwenu. Kama Maandiko Matakatifu yanavyosema: “Kila neno linapaswa kuhakikishwa kwa ushuhuda wa watu wawili au watatu.” Kwa wakati huu ninapokuwa mbali nanyi, ninarudilia kuwaambia waziwazi maneno yale niliyokuwa nimekwisha kuwaambia mbele katika safari yangu ya pili niliyofanya kwenu. Ninawaambia kwamba nitakapokuja kwenu mara tena, sitakosa kuazibu wale waliofanya zambi zamani na wengine wote. Nitafanya vile kwa sababu ninyi munataka uhakikisho kwamba Kristo anasema kwa njia yangu. Kwenu Kristo si zaifu, lakini anaonyesha uwezo wake kati yenu. Ni kweli Kristo alitundikwa juu ya musalaba katika hali ya uzaifu wa mwili, lakini sasa anaishi kwa uwezo wa Mungu. Nasi katika kuungana kwetu naye sisi vilevile tunakuwa zaifu. Lakini kwa ajili yenu tunaishi pamoja naye kwa nguvu ya Mungu. Mujichunguze ninyi wenyewe kusudi mupate kujua kama munasimama imara katika imani. Mujipime. Si munajua kwamba Yesu Kristo anakaa kati yenu? Kama si vile ni kusema kwamba mumeshindwa. Lakini ninatumaini kwamba ninyi mutajua kwamba sisi hatukushindwa. Nasi tunaomba Mungu kusudi musifanye jambo lolote baya, nasi hatutaki kuonyesha kwamba tumeshinda. Lakini tunataka mutende mema hata ikionekana kuwa sisi tunashindwa. Kwa maana hatuwezi kufanya jambo lolote linalopingana na ukweli. Jambo tunaloweza tu ni kuendelesha ukweli. Tunafurahi wakati ninyi munapokuwa na nguvu, hata ikiwa sisi ni zaifu. Nasi tunawaombea kusudi mupate kuwa wakamilifu. Ni kwa hiyo ninawaandikia maneno haya nikiwa mbali nanyi, kusudi wakati nitakapokuwa kati yenu nisitende kwa ukali kadiri ya mamlaka Bwana aliyonipa. Kwa maana uwezo ule ni kwa ajili ya kuwajenga katika imani, lakini si wa kubomoa. Basi kwa kumaliza, wandugu zangu, kwa heri. Mujikaze kuwa wakamilifu, mufarijiane ninyi kwa ninyi, mukuwe na nia moja, muishi katika amani, na Mungu wa upendo na amani atakuwa pamoja nanyi. Musalimiane kwa upendo wa kikristo. Watu wote wa Mungu wanawasalimia. Tunawatakia ninyi wote neema kutoka kwa Bwana Yesu Kristo, na upendo wa Mungu na ushirika wa Roho Mutakatifu. Tunawatakia neema na amani kutoka kwa Mungu Baba na kwa Bwana wetu Yesu Kristo. Kristo alijitoa mwenyewe kwa kutuokoa toka katika zambi zetu, kusudi atukomboe katika dunia hii mbaya ya sasa, kwa mapenzi ya Mungu Baba yetu. Mungu atukuzwe kwa milele na milele! Amina. Ninashangaa sana kuona namna gani munageuka hivi upesi kwa kumwacha yule aliyewaita kwa njia ya neema ya Kristo na kufuata habari njema ya namna ingine. Kwa kweli hakuna Habari Njema ingine, lakini kuko watu wanaowavuruga, wakitaka kugeuza Habari Njema ya Kristo. Lakini kama sisi wenyewe au malaika kutoka mbinguni, akiwahubiri ninyi Habari Njema inayokuwa mbalimbali na ile tuliyowahubiri, alaaniwe! Tumekwisha kuwaambia mambo haya zamani, nami ninayarudilia tena: mutu akiwahubiri habari njema inayokuwa mbalimbali na ile muliyopokea, alaaniwe! Basi kusema vile inaonyesha kwamba ninatafuta watu wanikubali? Hapana! Ninataka kukubaliwa na Mungu. Au ninatafuta kuwapendeza watu? Kama ningekuwa ningali ninatafuta kuwapendeza watu, singekuwa mutumishi wa Kristo. Wandugu zangu, ninawajulisha kwamba Habari Njema ninayohubiri haikutungwa na mutu. Sikuipokea kutoka kwa mutu wala sikuifundishwa na mutu, lakini ni Yesu Kristo aliyeifunua kwangu. Mumesikia namna mwenendo wangu ulivyokuwa zamani, wakati nilipofuata dini ya Kiyuda. Munajua namna nilivyotesa kanisa la Mungu vikali sana na kujikaza kwa kuliharibu. Nami niliendelea vizuri sana katika dini ya Kiyuda kuwapita watu wote wengine wa kabila langu wenye umri wangu, nikijikaza sana kushika desturi za babu zetu. Lakini, Mungu aliyenichagua mbele sijazaliwa na kuniita kwa neema yake, alipendezwa kumufunua Mwana wake kwangu, kusudi nihubiri Habari yake Njema kwa watu wa mataifa mengine. Na pale pale sikuomba shauri kwa mutu yeyote, wala sikwenda Yerusalema kwa kuonana na wale waliokuwa mitume mbele yangu, lakini nikajiendea katika inchi ya Arabia. Kisha nikarudia tena Damasiki. Kulipokwisha kupita miaka mitatu, nikaenda Yerusalema kusudi nipate kujuana na Petro, nami nikakaa kwake kwa muda wa siku kumi na tano. Sikumwona mutu mwingine isipokuwa tu Yakobo, ndugu ya Bwana. Ninaapa mbele ya Mungu kuwa sisemi uongo katika maneno haya ninayowaandikia. Nyuma ya pale nikaenda pande za jimbo la Suria na la Kilikia. Katika siku zile makanisa ya Yudea yalikuwa hayajaniona kwa uso, lakini yalikuwa yakisikia tu habari kwamba: “Yule aliyekuwa akitutesa zamani, sasa anahubiri habari za imani ile aliyokuwa akipotosha.” Nao yalimusifu Mungu kwa ajili yangu. Kulipokwisha kupita miaka kumi na mine, nikarudia Yerusalema pamoja na Barnaba; nami nilikuwa pamoja na Tito vilevile. Nilienda kule kufuatana na agizo nililopata katika maono. Halafu nikakusanyika na waongozi kwa upekee. Nikawaelezea Habari Njema ninayohubiri kati ya mataifa mbalimbali kusudi kazi yangu ya mbele au ya sasa isipotee bure. Na Tito aliyesafiri pamoja nami hakulazimishwa kutahiriwa ingawa alikuwa Mugriki, ijapokuwa wandugu wamoja wa uongo waliojiunga nasi kwa kisirisiri walitaka kumutahiri. Watu hao walijiingiza katika kikundi kusudi wapate kupeleleza jinsi tunavyoishi katika uhuru kutokana na kuungana kwetu na Yesu Kristo. Walitaka kututia katika maisha ya kitumwa. Lakini hatukukubali kuwatii watu wale hata kidogo, kusudi ukweli wa Habari Njema uendelee kuchungwa kati yenu siku zote. Lakini kuelekea wale waliohesabiwa kuwa waongozi, hainifalii kitu kujua cheo gani walichokuwa nacho, kwa maana Mungu hahukumu kwa kuangalia mambo ya inje. Watu wale hawakunifundisha kitu kipya. Lakini walitambua kuwa Mungu amenipatia kazi ya kuhubiri Habari Njema kwa watu wa mataifa mengine sawa alivyomupatia Petro kazi ya kuihubiri kwa Wayuda. Kwa maana yule aliyemuwezesha Petro kuwa mutume kwa Wayuda, ndiye aliyeniwezesha vilevile kuwa mutume kwa watu wa mataifa mengine. Basi Yakobo, Petro na Yoane, waliohesabiwa kuwa waongozi wakubwa, walitambua neema ile niliyojaliwa na Mungu wakatupatia mukono, mimi na Barnaba kuwa kitambulisho cha ushirika. Hivi tukapatana kwamba sisi tutakwenda kuhubiri watu wa mataifa mengine na wao watakwenda kuhubiri Wayuda. Lakini kitu kimoja walichotuomba ni kukumbuka wamasikini wa makanisa yao, nami nimefanya vile kwa bidii. Petro alipofika Antiokia, nilibishana naye waziwazi, kwa sababu alikuwa akidanganyika. Kwa maana mbele ya kufika kwa watu wamoja waliotumwa na Yakobo kule, yeye alizoea kula pamoja na watu wa mataifa mengine. Lakini watu wale walipofika, akajitenga na kuacha kula pamoja na watu wa mataifa mengine, kwa sababu ya kuogopa wale wanaolazimisha kutahiriwa. Na waamini wengine Wayuda wakaanza kutenda kwa unafiki sawa Petro, na hata Barnaba akajiunga nao katika huo unafiki wao. Wakati nilipoona kwamba walikuwa wakitembea kinyume cha ukweli wa Habari Njema, nikamwambia Petro hivi mbele ya watu wote: “Ikiwa wewe unayekuwa Muyuda unafuata desturi za watu wa mataifa mengine, namna gani unaweza kuwalazimisha watu wa mataifa mengine wafuate desturi za Wayuda?” Hakika sisi Wayuda wa kizalikio hatuko watu wa mataifa mengine, hao wenye zambi. Lakini, tunajua kwamba mutu hahesabiwi haki mbele ya Mungu kwa njia ya kushika Sheria, lakini kwa njia ya kuamini Yesu Kristo. Sisi vilevile tumeamini Yesu Kristo kusudi tupate kuhesabiwa haki kwa njia ya imani katika yeye, wala si kwa njia ya kushika Sheria. Ni vile kwa maana hakuna mutu atakayehesabiwa haki kwa njia ya kushika Sheria. Sasa tunapotafuta kuhesabiwa haki katika kuungana na Kristo, inaonekana kwamba sisi nasi ni wenye zambi sawa watu wa mataifa mengine. Jambo hili linaonyesha ya kama Kristo anatumika kwa ajili ya kuendelesha zambi? Hapana hata kidogo! Lakini ikiwa ninajenga tena kile nilichokwisha kubomoa, basi ninahakikisha kwamba mimi nimevunja Sheria. Maana kufuatana na Sheria hiyo, mimi nimekuwa kama mufu, na kifo kile kimesababishwa na Sheria. Imetokea vile kusudi nipate kuishi kwa ajili ya Mungu. Mimi nimekufa pamoja na Kristo juu ya musalaba. Na sasa si mimi ninayekuwa ningali nikiishi, lakini ni Kristo anayeishi ndani yangu. Maisha ninayoishi sasa, inatokana na kumwamini Mwana wa Mungu aliyenipenda na kutoa maisha yake kwa ajili yangu. Mimi sitaki kukataa neema ya Mungu kwa maana ikiwa wanaweza kuhesabiwa haki mbele ya Mungu, kwa njia ya kushika Sheria, basi Kristo alikufa bure. Ee ninyi Wagalatia! Ninyi wajinga! Ni nani aliyewaloga? Habari juu ya kutundikwa kwa Yesu Kristo juu ya musalaba ilielezwa waziwazi mbele ya macho yenu. Ninataka mujibu ulizo hili moja: mumepokea Roho wa Mungu kwa sababu ya kushika Sheria au kwa sababu mumesikia na kuamini Habari Njema? Namna gani mumekuwa wajinga hivi? Ninyi mumeanza mambo yote kwa nguvu za Roho wa Mungu, sasa munataka kuyatimiza kwa nguvu za kimwili? Mambo yote yaliyowatokea ninyi, yalikuwa ya bure? Hakika hayakukuwa ya bure. Mungu aliwajaza Roho wake na kufanya miujiza kati yenu kwa sababu munashika Sheria au kwa sababu munasikia na kuamini Habari Njema? Hivyo “Abrahamu alimwamini Mungu, na kwa hiyo akahesabiwa kuwa mwenye haki.” Basi mutambue kwamba wazao wa kweli wa Abrahamu ni wale wanaokuwa wenye imani. Vilevile Maandiko Matakatifu yalisema tangu zamani kwamba watu wa mataifa mengine watahesabiwa haki mbele ya Mungu kwa njia ya imani yao. Kwa sababu Mungu alipasha kwanza Habari Njema hii kwa Abrahamu: “Kwa njia yako mataifa yote yatabarikiwa.” Kufuatana na hiyo, Mungu atawabariki wote wanaoamini sawa vile alivyomubariki Abrahamu, mwenye imani. Lakini wale wanaotegemea kutimiza yale yanayoamuriwa na Sheria, wamelaaniwa. Kwa maana Maandiko Matakatifu yanasema: “Alaaniwe mutu yeyote asiyedumu katika yote yanayoandikwa katika hiki kitabu cha Sheria na kuyatii.” Na zaidi ya hii ni wazi kwamba hakuna mutu anayehesabiwa haki mbele ya Mungu kwa njia ya Sheria. Kwa maana Maandiko Matakatifu yanasema: “Mwenye haki ataishi kwa njia ya imani.” Na tena hakuna ushirika kati ya Sheria na imani. Lakini Maandiko Matakatifu yanasema: “Yule anayeshika maagizo ya Sheria hii ataishi kwa njia hiyo.” Kristo alitukomboa toka laana ya Sheria, akijitwalia laana hiyo kwa ajili yetu. Kwa maana Maandiko Matakatifu yanasema: “Mutu yeyote anayetundikwa juu ya muti amelaaniwa.” Ilitendeka hivi kusudi kwa njia ya Yesu Kristo, baraka Mungu aliyoahidi kwa Abrahamu itolewe vilevile kwa watu wa mataifa mengine na hata sisi kwa njia ya imani, tupate kupokea yule Roho aliyeahidiwa na Mungu. Wandugu, nitatumia mufano huu wa kawaida: mutu anapofanya agano kwa njia ya haki, hakuna mutu anayeweza kulivunja au kuongeza neno lingine juu yake. Basi, Mungu alitoa ahadi kwa Abrahamu na uzao wake. Maandiko hayasemi kwamba alitoa ahadi zile kwa “wazao wake” kama vile angeitoa kwa watu wengi. Lakini yanasema kwamba “kwa uzao wako”, maana yake kwa mutu mumoja tu ndiye Kristo. Mambo ninayotaka kusema ni haya: Mungu amekwisha kufanya agano kwa njia ya haki. Nayo Sheria iliyotokea miaka mia ine makumi tatu nyuma yake haiwezi kulivunja au kugeuza ile ahadi ya Mungu. Lakini, kama zawadi ya Mungu inatokana na Sheria, basi, haiwezi kutokana tena na ahadi. Lakini kwa njia ya ahadi, Mungu ameonyesha wema wake kwa Abrahamu. Basi Sheria iko na kazi gani? Ilisimamishwa nyuma kwa ajili ya kutambulisha makosa. Nayo ilipaswa kuendelea mpaka atakapokuja yule muzao wa Abrahamu ambaye Mungu alikuwa ameahidi. Sheria hii ilitangazwa na malaika kwa njia ya mupatanishi. Lakini ikiwa jambo linaelekea mutu mumoja tu, si lazima kuwa na mupatanishi; na Mungu ni mumoja tu. Basi, ni kusema kwamba Sheria haipatani na ahadi za Mungu? Hapana, hata kidogo! Kama kungetolewa Sheria yenye uwezo wa kuleta uzima kwa watu, basi mutu angehesabiwa haki mbele ya Mungu kwa njia ya Sheria. Lakini Maandiko Matakatifu yanasema kwamba watu wote wako chini ya utumwa wa zambi, kusudi zawadi iliyoahidiwa na Mungu itolewe kwa wale wanaoamini kwa njia ya imani yao katika Yesu Kristo. Wakati wa imani ulipokuwa haujatokea, tulichungwa na Sheria, kama vile wafungwa, tukingojea mpaka imani ile ifunuliwe. Hivi Sheria ilikuwa kama mwangalizi wetu mpaka Kristo alipofika, kusudi tuhesabiwe haki mbele ya Mungu kwa njia ya imani. Lakini tangia kufika kwa imani, sisi hatuko tena chini ya uangalizi ule. Kwa maana ninyi wote mumekuwa wana wa Mungu kwa njia ya imani na kuungana na Yesu Kristo. Hivi, ninyi wote mulioungana na Yesu Kristo, kwa njia ya kubatizwa, ni kama vile mumevaa Kristo. Kwa hiyo hakuna tena umbalimbali kati ya Wayuda na watu wa mataifa mengine, kati ya watumwa na watu huru, mwanaume na mwanamuke; kwa maana ninyi wote ni mumoja katika kuungana kwenu na Yesu Kristo. Kama ninyi ni watu wa Kristo, basi, ninyi ni wazao wa Abrahamu, ninyi mutakuwa warizi sawa vile Mungu alivyoahidi. Mimi ninataka kusema hivi: mwana anayepaswa kurizi mali ya baba yake anatendewa kama mutumwa kwa muda wote anapokuwa angali mudogo, ijapokuwa yeye ndiye kweli mwenyeji wa mali yote. Kwa muda ule yeye ni chini ya madaraka ya watu wanaomuchunga na ya walinzi wa mali mpaka wakati baba yake aliopanga upate kutimia. Na sisi vilevile tulipokuwa tungali kama watoto, tulikuwa watumwa wa vitu vyenye uwezo vilivyotawala dunia. Lakini wakati uliopangwa ulipotimia, Mungu akamutuma Mwana wake: akazaliwa na mwanamuke na kuishi chini ya uongozi wa Sheria, kusudi awakomboe wale walioishi chini ya uongozi wa Sheria. Alifanya vile kusudi tupate kuwa wana wa Mungu. Mungu alituma Roho wa Mwana wake ndani ya moyo wetu kwa kuhakikisha ya kuwa ninyi ni wana wake. Roho anayetuombea, akiita: “Baba!” Basi wewe si mutumwa tena, lakini mwana, na kwa kuwa wewe ni mwana wake, Mungu atakupa sehemu ya urizi aliouahidi kwa wana wake. Zamani, mulipokuwa hamumujui Mungu, mulikuwa watumwa wa miungu isiyokuwa ya kweli. Lakini sasa munamujua Mungu, au afazali tuseme kwamba sasa munajulikana naye. Basi namna gani mumerudilia tena vitu vinavyotawala dunia, visivyokuwa na uwezo na vikosefu, mukitaka kuwa watumwa tena? Kwa nini munashugulika na kutimiza desturi zenu za siku, miezi, nyakati na za miaka? Ninawaogopea, kwa maana inawezekana kwamba nimesumbuka bure kwa ajili yenu! Wandugu zangu, ninawasihi mukuwe kama mimi, kwa kuwa mimi nimekuwa kama ninyi. Ninyi hamukunitendea ubaya wowote. Munakumbuka kwamba niliwahubiri Habari Njema kwa mara ya kwanza kwa sababu ya ugonjwa nilioupata. Mulipata majaribu kwa sababu ya hali ya mwili wangu. Ingawa hivi hamukunizarau wala kuchukizwa nami, lakini mulinipokea sawa vile mungepokea malaika wa Mungu au Yesu Kristo! Ninyi mulikuwa wenye furaha. Sasa nini imewatokea? Kwa maana ninaweza kuwashuhudia kwamba mungeweza kuongoa hata macho yenu na kuyatoa kwangu! Basi nimegeuka sasa adui yenu kwa sababu ya kuwaambia ukweli? Wale watu wanaonyesha kwamba wanawashugulikia, lakini nia yao si nzuri. Wao wanataka kuwatenganisha na mimi, kusudi mupate kushugulika nao. Ni vizuri kushugulika na mambo mema siku zote, wala si wakati ninapokuwa pamoja nanyi tu. Watoto wangu wapendwa, kama vile mwanamuke anavyopata uchungu wa kuzaa, mimi vilevile, ninapata tena uchungu kwa ajili yenu mpaka mutakapokuwa na hali inayokuwa kama ya Kristo ndani yenu. Ningependa kuwa pamoja nanyi sasa, kwa maana ningetumia usemi mwingine. Ninashikwa na wasiwasi kwa ajili yenu. Muniambie ninyi munaotaka kuishi chini ya Sheria, hamujui vile Sheria inavyosema? Imeandikwa kwamba Abrahamu alikuwa na wana wawili. Alizaa mwana mumoja na muke wake mujakazi na mwingine na muke wake huru wa ndoa. Yule mwana wa mujakazi alizaliwa sawa kawaida, lakini yule wa muke huru alizaliwa kutokana na ahadi ya Mungu. Maneno haya ni kama vile mufano: wake hawa wawili ni mufano wa maagano mawili. Yule Hagari, watoto wake waliozaliwa katika hali ya utumwa, ni mufano wa agano lililofanyika kwenye mulima Sinai. Hagari analinganishwa na mulima Sinai wa inchi ya Arabia, na ni mufano wa Yerusalema ya sasa, unaokuwa katika utumwa pamoja na wakaaji wake. Lakini Yerusalema ya mbinguni ni huru, nao ni mama yetu. Kwa maana Maandiko Matakatifu yanasema: “Ufurahi wewe tasa, ushangilie, upige kelele wewe usiyejua uchungu wa kuzaa. Kwa maana muke aliyeachwa na mume, atakuwa na watoto wengi kuliko yule anayekuwa naye.” Nanyi wandugu ni watoto wa Mungu waliozaliwa kutokana na ahadi yake kama vile Isaka. Zamani mutoto aliyezaliwa sawa kawaida alimutesa yule aliyezaliwa kwa uwezo wa Roho wa Mungu, na ingali inafanyika vile hata sasa. Lakini Maandiko Matakatifu yanasema nini? Yanasema: “Fukuza mujakazi huyu pamoja na mwana wake; kwa maana mwana wa mujakazi hatarizi pamoja na mwana wa muke huru.” Hivi wandugu, sisi hatuko watoto wa mujakazi, lakini sisi ni watoto wa muke huru. Kristo ametukomboa katika utumwa kusudi tukuwe huru kabisa. Basi, musimame imara wala musijitie tena katika vifungo vya utumwa. Musikilize! Mimi Paulo ninataka kuwaambia kwamba kama mukikubali kutahiriwa, Kristo hana mafaa yoyote kwenu. Mimi ninasema tena wazi, kila mutu anayekubali kutahiriwa sherti ashike Sheria yote. Kama munatafuta kuhesabiwa haki mbele ya Mungu kwa njia ya kushika Sheria, mumejitenga mbali na Kristo na kujipotezea neema ya Mungu. Lakini sisi tunangojea kwa matumaini kwamba kwa uwezo wa Roho, tutahesabiwa haki kwa njia ya imani. Kwa maana kwa wale wanaoungana na Kristo Yesu, kutahiriwa au kutokutahiriwa hakufai kitu. Kitu kinachofaa ni imani inayotenda kazi kwa upendo. Ninyi mulikuwa na mwenendo muzuri! Ni nani aliyewazuiza kushika ukweli? Kishawishi hicho hakikutoka kwa Mungu anayewaita ninyi kuwa watu wake. “Chachu kidogo inachachisha donge zima.” Ingawa vile mimi niko na tumaini juu yenu kutoka kwa Bwana kwamba hamutakuwa na nia mbalimbali na mimi. Lakini yule anayewavuruga ataazibiwa hata ikiwa ni nani. Wandugu, ikiwa mimi ningali ninahubiri ya kama ni lazima kutahiriwa, basi kwa sababu gani ningali ninateswa? Kama ningefanya vile, basi watu hawangechukizwa na mahubiri yangu juu ya musalaba wa Kristo. Heri wale wanaoleta fujo kati yenu wangejikata viungo vyao vya uzazi. Wandugu, ninyi muliitwa na Mungu kusudi mukuwe watu huru. Basi musitumie uhuru huu kuwa ruhusa ya kutimiza tamaa za mwili, lakini musaidiane kwa upendo. Kwa maana Sheria yote inafungwa katika amri hii moja: “Umupende mwenzako kama unavyojipenda mwenyewe.” Lakini kama mukiumana na kukulana kama nyama wa pori, muangalie vizuri musiteketezane. Mambo ninayotaka kusema ni haya: muishi chini ya uongozi wa Roho Mutakatifu, nanyi musitimize tamaa za kimwili. Kwa maana tamaa za kimwili zinapingana na tamaa za Roho Mutakatifu. Na tamaa za Roho zinapingana na tamaa za kimwili. Hao wawili wanapingana hata munashindwa kufanya sawa vile munavyotaka. Lakini kama mukiongozwa na Roho Mutakatifu, hamutaishi tena chini ya Sheria. Matendo ya kimwili yanajulikana wazi, nayo ndiyo uasherati, uchafu, kutawaliwa na tamaa za kimwili, kutambikia sanamu, uchawi, uadui, ugomvi, wivu, kasirani, mapingano, matengano, ubaguzi, chuki, uuaji, ulevi, ulafi, na mambo mengine yanayofanana na hayo. Ninawaonya tena kama vile nilivyowaonya mbele, kwamba watu wanaotenda mambo kama hayo hawatashiriki katika Ufalme wa Mungu. Lakini tunda la Roho ni upendo, furaha, amani, uvumilivu, wema, fazili, uaminifu, upole na kujizuiza. Hakuna Sheria inayokataza mambo kama hayo! Nao watu wa Kristo Yesu wameua hali yao ya kimutu pamoja na vifungo vyao vyote na tamaa zote mbaya. Kufuatana na vile tunavyoishi kwa nguvu za Roho, basi tufuate maongozi ya Roho vilevile. Tusijivune, tusichokozane wala kuoneana wivu. Wandugu zangu, kama mutu akipatikana na kosa fulani, ninyi munaoongozwa na Roho wa Mungu mumwonye mutu yule kwa roho ya upole. Na kila mumoja wenu ajiangalie mwenyewe, kusudi asijaribiwe vilevile. Musaidiane ninyi kubeba mizigo yenu, na hivi mutatimiza sheria ya Kristo. Kama mutu akijizania kwamba yeye ni kitu, ijapokuwa yeye si kitu, anajidanganya yeye mwenyewe. Kila mutu achunguze mwenendo wake mwenyewe. Basi akiwa na sababu ya kujivuna, ajivune kufuatana na mwenendo wake mwenyewe pasipo kujilinganisha na mutu mwingine. Kwa maana kila mutu anapaswa kubeba muzigo wake mwenyewe. Mwenye kufundishwa Habari Njema anapaswa kushirikiana mapato yake na yule anayemufundisha. Musidanganyike: Mungu hachekelewi. Chochote mutu atakachopanda, ndicho atakachovuna. Anayepanda kwa kupendeza hali yake ya kimwili, atavuna matunda yanayotokana na hali ile, nayo ni lufu. Lakini anayepanda kwa kupendeza Roho Mutakatifu, atavuna matunda yanayotokana na Roho yule, nayo ni uzima wa milele. Tusichoke kutenda mema; kwa maana siku zitakapotimia tutavuna kama tusiporegea. Basi, tunapokuwa bado na wakati, tufanye mema kwa watu wote, na zaidi kwa wandugu zetu katika imani. Mujionee wenyewe ni kwa herufi kubwa gani nimewaandikia ninyi kwa mukono wangu mwenyewe! Wale watu wanaowalazimisha ninyi kutahiriwa, ndio wanaotaka kujionyesha katika mambo yanayoelekea mwili. Lakini wanafanya vile tu kusudi wasiteswe kwa ajili ya kuhubiri habari za musalaba wa Kristo. Watu hao wanaotahiriwa, hawashiki Sheria lakini wanataka mutahiriwe kusudi wapate kujivuna kwamba wanawashurutisha kuwa na kitambulisho kile juu ya mwili wenu. Na mimi kwa ngambo yangu sitaki kujivuna, isipokuwa tu kwa ajili ya musalaba wa Bwana wetu Yesu Kristo. Maana kwa njia ya musalaba huo, ninahesabu dunia kama vile imekwisha kufa na mbele ya dunia mimi ninahesabiwa kama vile mufu. Kutahiriwa au kutokutahiriwa hakufai kitu; kitu cha lazima ni kuwa kiumbe kipya. Na wote wanaofuata kanuni hii katika maisha yao pamoja na watu wa Mungu wanaohesabiwa kama Waisraeli wa kweli, ninawatakia amani na wema. Basi sasa, mutu asinisumbue tena kwa maana niko na makovu juu ya mwili wangu niliyopata kwa ajili ya Yesu. Wandugu, ninawatakia ninyi wote neema kutoka kwa Bwana wetu Yesu Kristo. Amina. Barua hii inatoka kwangu mimi Paulo. Mimi niliyeitwa kwa mapenzi ya Mungu kuwa mutume wa Yesu Kristo. Ninawaandikia ninyi watu wa Mungu munaokaa Efeso, munaokuwa waaminifu katika kuungana na Yesu Kristo. Ninawatakia neema na amani toka kwa Mungu Baba yetu na kwa Bwana Yesu Kristo. Asifiwe Mungu, Baba ya Bwana wetu Yesu Kristo! Yeye ndiye aliyetupatia baraka za kiroho za kila namna kutoka katika eneo la mbingu kwa njia ya kuungana kwetu na Kristo. Mbele ya kuumbwa kwa dunia, Mungu alituchagua kuwa watu wake kwa njia ya kuungana kwetu na Kristo, kusudi tukuwe watakatifu na pasipo kilema mbele yake. Kwa sababu ya upendo wake, Mungu amekusudia tangu zamani kutukubali sisi kuwa watoto wake kwa njia ya Yesu Kristo. Alifanya vile kufuatana na mapenzi yake. Basi tumusifu Mungu kwa sababu ya utukufu wa neema yake aliyotujalia kwa njia ya Mwana wake mupendwa. Kwa njia ya damu ya Kristo, sisi tumekombolewa, maana yake zambi zetu zimesamehewa. Hivi Mungu ameonyesha uwingi wa neema yake akitupatia hekima na akili kamili. Ametujulisha mipango yake iliyokuwa imefichwa; ndiyo ile aliyokusudia kwa mapenzi yake tangu mbele kwamba ataitimiza kwa njia ya Kristo. Kusudi la mupango ule utakaotimia kwa wakati uliowekwa, ni kukusanya viumbe vyote vinavyokuwa mbinguni na katika dunia chini ya utawala wa Kristo. Mungu amefanya kila kitu kufuatana na kusudi na mapenzi yake. Yeye ametuchagua kwa njia ya kuungana kwetu na Kristo, kusudi tukuwe watu wake. Kwa hiyo sisi tuliotangulia kumutumainia Kristo, tumusifu Mungu kwa ajili ya utukufu wake! Ninyi vilevile, wakati muliposikia ujumbe wa kweli, maana yake Habari Njema iliyowaletea wokovu, mukamwamini Kristo. Naye Mungu akawapatia Roho Mutakatifu aliyeahidi kuwa kitambulisho cha kuhakikisha kwamba ninyi ni watu wake kabisa. Yule Roho ni rehani ya urizi aliowawekea watu wake. Na jambo hili linahakikisha kwamba Mungu atakomboa kabisa wote wanaokuwa wake. Tumusifu kwa ajili ya utukufu wake. Kwa sababu hiyo, tangu niliposikia namna munavyomwamini Bwana Yesu na namna munavyowapenda watu wote wa Mungu, mimi sichoki kumushukuru Mungu kwa ajili yenu. Ninawakumbuka katika maombi yangu. Ninamwomba Mungu wa Bwana wetu Yesu Kristo, Baba mwenye utukufu, awapatie Roho wake kusudi mukuwe na hekima na ufunuo hata muweze kumujua. Ninaomba Mungu aifungue mioyo yenu ipate kuona mwangaza wake. Kwa hiyo mutapata kujua tumaini munalokuwa nalo kutokana na mwito wa Mungu. Vilevile mupate kujua utajiri mukubwa wa urizi anaouwekea watu wake, na kutambua jinsi uwezo wake unavyokuwa mukubwa sana kwa ajili yetu sisi waamini, akizitumia nguvu zake kubwa sana. Alifanya vile wakati alipomufufua Kristo na kumwikalisha na mamlaka kwa kuume kwake mbinguni. Na kule anatawala juu ya wakubwa wote, wenye mamlaka wote, wenye uwezo wote na wasultani wote na juu ya kila cheo kinachoweza kuwa katika dunia hii na katika dunia itakayokuja. Mungu amemupatia Kristo mamlaka juu ya vitu vyote na kumuweka kuwa kichwa cha kanisa. Kanisa ni mwili wa Kristo, nalo ni utimilifu wa Kristo anayetimiza vitu vyote. Zamani ninyi mulikuwa mumekufa kiroho kwa sababu ya makosa na zambi zenu. Mulikuwa mukiishi kufuatana na mwenendo mubaya wa dunia hii. Mulitii mutawala wa roho zenye uwezo wa anga anayetawala sasa watu wasiomutii Mungu. Zamani, sisi wote vilevile tulikuwa kama wao. Tuliishi kufuatana na tamaa zetu za kimwili na kutenda kufuatana na mapenzi ya mwili na roho zetu. Kwa sababu ya hali yetu ya kimwili, hatungeponyoka kasirani ya Mungu kama wengine. Lakini Mungu ni mwenye huruma nyingi. Alitupenda kwa upendo wake mukubwa; sisi tuliokuwa tumekufa kwa sababu ya makosa yetu, alitufufua pamoja na Kristo. Hivi mumeokolewa kwa neema ya Mungu. Katika kuungana kwetu na Yesu Kristo, Mungu ametufufua pamoja naye kusudi tutawale pamoja naye mbinguni. Alifanya vile kusudi aonyeshe kwa vizazi vyote vitakavyokuja neema yake kubwa ya ajabu kwa njia ya wema wake katika kuungana kwetu na Yesu Kristo. Kwa maana mumeokolewa kwa neema ya Mungu, kwa njia ya imani. Jambo hili halitokani na ninyi wenyewe, lakini ni zawadi ya Mungu. Si kwa matendo yenu, kusudi mutu asipate kujivuna. Kwa maana sisi ni viumbe vya Mungu, na kwa kuungana kwetu na Yesu Kristo, alituumba kusudi tuishi maisha ya matendo mema, ambayo Mungu alitutayarishia tangu mbele tupate kuyatenda. Basi mukumbuke namna mulivyokuwa zamani ninyi munaokuwa kwa kizalikio watu wa mataifa mengine. Wayuda wanawaita ninyi watu wasiotahiriwa, lakini wao wanajiita wenye kutahiriwa kwa sababu ya kitambulisho cha kutahiriwa na watu katika miili yao. Kwa wakati ule mulikuwa mumetengwa mbali na Kristo. Hamukukuwa kati ya watu waliochaguliwa na Mungu, mulikuwa wageni kati yao. Ninyi hamukukuwa na pato lolote katika agano zile Mungu alizotoa katika ahadi yake kwa watu wake. Muliishi katika dunia pasipo tumaini wala kumujua Mungu. Lakini sasa, katika kuungana kwenu na Yesu Kristo, ninyi muliokuwa mbali, mumekuwa karibu kwa njia ya damu ya Kristo. Kwa maana Kristo mwenyewe ndiye aliyetuletea amani akifanya Wayuda na watu wa mataifa mengine kuwa jamii moja. Kwa njia ya kutoa mwili wake, amevunja uadui uliokuwa kama ukuta uliowatenganisha. Yeye aliondoa Sheria ya Kiyuda pamoja na amri zake na maagizo yake akifanya watu wa jamii hizi mbili kuwa watu wa taifa moja jipya katika kuungana naye na kuleta amani. Kristo alivunja uadui kwa njia ya kufa kwake juu ya musalaba, akaunganisha watu wa makabila haya mawili kuwa moja na kuwapatanisha na Mungu. Hivi, Kristo amekuja kutangaza Habari Njema ya amani kwa ninyi watu wa mataifa mengine, muliokuwa mbali na Mungu, na kwa Wayuda waliokuwa karibu naye. Kwa maana, kwa njia ya Kristo sisi wote, Wayuda na watu wa mataifa mengine, tumefunguliwa njia ya kufika mbele ya Baba katika Roho mumoja. Basi sasa, ninyi watu wa mataifa mengine si wageni tena wala wapangaji. Lakini sasa mumekuwa wanainchi pamoja na watu wa Mungu na tena mumekuwa watu wa jamaa la Mungu. Ninyi vilevile ni kama jengo linalosimama juu ya musingi uliowekwa na mitume na manabii; Yesu Kristo mwenyewe ndiye jiwe kubwa la pembe. Katika kuungana naye, jengo lote nzima linaunganishwa vizuri na kuongezeka hata lipate kuwa hekalu takatifu kwa ajili ya Bwana. Katika kuungana pamoja na Kristo, ninyi vilevile munaunganishwa pamoja na wengine wote kuwa makao ya Mungu kwa njia ya Roho wake. Kufuatana na mambo hayo, mimi Paulo, mufungwa wa Yesu Kristo kwa ajili yenu ninyi watu wa mataifa mengine, ninamwomba Mungu. Hakika, mumesikia jinsi Mungu alivyonijalia neema, akinipatia kazi ya kufanya kwa ajili yenu. Mungu amenijulisha kwa njia ya ufunuo mupango wake uliofichwa. (Nimekwisha kuwaandikia kwa kifupi juu ya maneno haya. Nanyi mukiyasoma mutaweza kutambua jinsi ninavyoelewa ule mupango wa Kristo uliofichwa.) Zamani, Mungu hakuwajulisha watu mupango ule sawa vile ameujulisha sasa kwa mitume na manabii wake watakatifu kwa njia ya Roho wake. Nao mupango ule ni kwamba kwa njia ya Habari Njema watu wa mataifa mengine wanapewa sehemu yao ya urizi kutoka kwa Mungu pamoja na Wayuda. Watu wale ni viungo vya mwili mumoja, nao wanapokea vilevile sehemu ya vitu Mungu alivyoahidi kwa njia ya Yesu Kristo. Nimewekwa kuwa mutumishi wa Habari Njema kwa njia ya zawadi Mungu aliyonipatia kutokana na uwezo wake. Mimi ni mudogo kuliko watu wote wa Mungu, lakini Mungu amenijalia neema ya kutangaza kwa watu wa mataifa mengine Habari Njema ya baraka za Kristo zisizoweza kuhesabiwa. Na hivi nipate kuwaelezea vema namna unavyotimia ule mupango uliokuwa umefichwa tangu zamani na Mungu, muumbaji wa vitu vyote. Lakini sasa, kwa njia ya kanisa, watawala na wote wenye uwezo wanaokuwa katika eneo la mbingu wapate kutambua hekima ya Mungu inayokuwa ya namna nyingi. Mungu amefanya hivi kufuatana na kusudi lake la milele alilofanya kwa njia ya Yesu Kristo Bwana wetu. Na katika kuungana kwetu na Yesu Kristo na kwa njia ya kumwamini tunapata uhuru wa kufika mbele ya Mungu tukiwa na tumaini kubwa. Basi ninawaomba musiregee kwa sababu ya mateso ninayopata kwa ajili yenu, kwa maana yanawaletea utukufu. Kwa sababu hiyo ninapiga magoti mbele ya Baba Mungu, anayekuwa asili ya jamaa zote zinazokuwa mbinguni na katika dunia. Ninaomba Mungu, kwa uwingi wa utukufu wake, awajalie nguvu mupate kuwa imara ndani ya roho zenu, kwa njia ya Roho wake. Hivi Kristo apate kukaa ndani ya mioyo yenu kwa njia ya imani, nanyi mupate kuwa na mizizi na musingi katika upendo. Kwa hiyo ninyi pamoja na watu wote wa Mungu mutaweza kutambua katika ngambo zote ukubwa wa upendo wa Kristo unaopita kipimo. Mutafikia kweli kutambua upendo wake, ijapokuwa unapita ufahamu wa watu wote, nanyi mutapata kuwa watimilifu kabisa sawa vile Mungu anavyokuwa. Basi, Mungu ambaye kwa nguvu yake inayofanya kazi ndani yetu, anaweza kufanya mambo makubwa zaidi yanayopita yale tunayoweza kuomba au kufikiri; atukuzwe katika kanisa na katika Yesu Kristo, kwa vizazi vyote kwa milele na milele. Amina. Kwa hivi basi, mimi ninayekuwa mufungwa kwa sababu ninamutumikia Bwana, ninawasihi muishi sawa inavyostahili kufuatana na mwito Mungu aliowatolea. Mukuwe wanyenyekevu kabisa, wapole na wavumilivu. Muvumiliane ninyi kwa ninyi kwa upendo. Mujikaze sana kuchunga umoja wa Roho, kwa amani inayowaunganisha. Kuna mwili mumoja na Roho mumoja, vilevile kuna tumaini moja la mwito muliotolewa na Mungu. Kuna Bwana mumoja, imani moja, ubatizo mumoja; Mungu mumoja, Baba ya watu wote, anayekuwa juu ya wote, anayetumika kwa njia ya wote, na anayekaa ndani ya wote. Lakini kila mutu kati yetu alipokea neema kadiri ya kipimo alichojaliwa na Kristo. Kama vile Maandiko Matakatifu yanavyosema: “Alipopanda juu, alikamata wafungwa, aliwapatia watu zawadi.” Basi, neno hili “alipanda juu,” lina maana gani? Maana yake ni kusema kwamba alishuka kwanza mpaka chini katika dunia. Yule aliyeshuka ndiye yule yule aliyepanda juu sana kupita mbingu zote kusudi akamilike katika ulimwengu wote. Ni yeye ndiye aliwapatia watu zawadi za kipekee. Amewaweka wamoja kuwa mitume, wengine kuwa manabii, wengine kuwa watangazaji wa Habari Njema, wengine kuwa wachungaji na walimu. Yeye amefanya vile kwa kuwatayarisha watu wa Mungu kwa kazi ya utumishi kusudi mwili wa Kristo upate kujengwa. Hivi, sisi wote tutafikia umoja wa imani yetu na wa kumujua kabisa Mwana wa Mungu; tutapata kukomaa na kufikia kipimo cha utimilifu wa Kristo. Basi, hatutakuwa tena kama watoto, tukipeperushwa na kuvutwa na mafundisho ya kila aina yanayoletwa na watu wanaodanganya wengine na kuwapotosha kwa mayele yao. Lakini tukitangaza ukweli kwa upendo, tutakomaa katika mambo yote na kufikia kuwa kama Kristo, ambaye ni kichwa. Kwa uongozi wake, viungo vyote vya mwili vinashikamana kabisa, nao mwili wote muzima unashikamana vizuri kwa nguvu ya maunganio yake. Halafu, kila kiungo kinapotumika kama kinavyopaswa, mwili wote unakomaa na kujijenga katika upendo. Basi, kwa jina la Bwana ninawaonya hivi: musiishi tena kama watu wa mataifa mengine, wanaofuata mawazo yao ya bure na wenye mafikiri yaliyotiwa katika giza. Watu hawa hawashiriki katika uzima ule unaoletwa na Mungu, kwa sababu wao ni wapumbafu na wenye mioyo migumu. Hawasikii tena haya hata kidogo nao wamejitoa katika mambo ya ovyo na kufanya bila kujizuiza mambo yote mabaya. Lakini ninyi hamukujifunza vile juu ya Kristo! Hakika mumesikia habari zake, nanyi mukiwa waamini mumefundishwa kufuatana na ukweli unaokuwa ndani ya Kristo. Basi munapaswa kutupilia mbali ile hali yenu ya zamani, ule utu wenu wa zamani unaopotoka kufuatana na tamaa zake za udanganyifu. Inafaa mufanywe upya katika roho zenu na katika nia zenu. Mukuwe na hali mupya, inayoumbwa kwa mufano wa Mungu na inayoonekana katika maisha ya haki na utakatifu wa kweli. Kwa hivi, muache uongo! Kila mumoja aseme ukweli kwa mwenzake, kwa maana sisi wote ni viungo vya mwili mumoja. Kama mukikasirika, musianguke katika zambi, kasirani yenu isidumu muchana kutwa, wala musimufungulie Shetani mulango. Yule aliyekuwa akiiba, asiibe tena, lakini ajikaze kufanya kazi peke yake kwa usawa kusudi apate kuwasaidia wakosefu. Musiseme neno lolote baya, lakini kama ni lazima museme tu maneno mazuri na ambayo yanasaidia kuwajenga wengine na yanayoleta neema kwa wale wanaoyasikia. Musihuzunishe Roho Mutakatifu wa Mungu; kwa maana Roho ni kitambulisho kilichowekwa juu yenu kwa kuhakikisha kwamba ninyi ni watu wake mpaka siku Mungu atakapowakomboa. Mutupilie mbali nanyi nia zote za uadui, chuki, kasirani, fujo na masingizio. Mutupilie mbali ubaya wa kila namna! Lakini mutendeane wema ninyi kwa ninyi; musameheane kama Mungu alivyowasamehe ninyi kwa njia ya Kristo. Mufuate tabia ya Mungu kwa maana ninyi ni watoto wake wapendwa. Muishi katika upendo kama vile Kristo alivyotupenda na kutoa maisha yake kwa ajili yetu kama vile matoleo na sadaka ya kuteketezwa kwa moto yenye harufu nzuri inayomupendeza Mungu. Kama vile inavyowapasa watu wa Mungu kuishi, tendo lolote la uasherati, la uchafu wala la tamaa ya mali lisisikilike kati yenu. Vilevile kusisikilike maneno ya matusi ya ovyo ovyo wala machafu, kwa maana hayana mafaa. Kinachofaa ni kumushukuru Mungu. Mujue waziwazi kwamba mwasherati yeyote na muchafu na mwenye tamaa ya mali (mwenye tamaa ni kama mwenye kuabudu sanamu), hao wote hawatapewa sehemu ya urizi katika Ufalme wa Kristo na Mungu. Mutu asiwadanganye na maneno yasiyokuwa na maana; kwa sababu ya makosa kama hayo, Mungu anawaazibu kwa kasirani yake wale wasiomutii. Basi musishirikiane na watu kama wale. Zamani muliishi katika giza, lakini sasa, kwa kuungana kwenu na Bwana, munaishi katika mwangaza. Muishi kama watoto wa mwangaza, kwa maana matunda ya mwangaza ni wema wa kila namna, haki na ukweli. Mujikaze kutambua mambo yanayomupendeza Bwana. Musishiriki katika matendo ya giza yasiyofaa, lakini muyafichue. (Kwa maana ni haya kusema juu ya mambo watu hao wanayofanya kwa siri.) Lakini matendo yale yote yanapofunuliwa katika mwangaza, yanaonekana wazi. Kwa maana yote yanayoonekana wazi yanageuka mwangaza. Ni kwa hiyo inasemwa hivi: “Amuka wewe unayelala! Ufufuke kutoka kati ya wafu, naye Kristo atakuangazia.” Muangalie vizuri mwenendo wenu. Musiishi kama wajinga lakini muishi kama wenye hekima. Mutumie vema wakati huu munaokuwa nao kwa maana siku hizi ni mbaya. Kwa hiyo musikuwe wajinga, lakini mutambue mapenzi ya Bwana. Musilewe divai kwa maana inaleta upotovu, lakini mujazwe na Roho. Munapoongea, museme maneno ya zaburi, mumusifu Bwana na kumwabudu kwa nyimbo za kiroho. Mumwimbie na kumushangilia kwa moyo wenu wote. Mumushukuru Mungu Baba siku zote kwa kila jambo, kwa jina la Bwana wetu Yesu Kristo. Mukuwe na utii ninyi kwa ninyi kwa kumuheshimu Kristo. Wake wawatii waume wao kama vile wanavyomutii Bwana. Kwa maana mume ni kichwa cha muke wake, kama vile Kristo anavyokuwa kichwa cha kanisa. Naye mwenyewe ni Mwokozi wa kanisa ambalo ni mwili wake. Wake wanapaswa kutii waume wao katika kila jambo sawa vile kanisa linavyomutii Kristo. Nanyi waume muwapende wake wenu sawa vile Kristo alivyopenda kanisa na kutoa uzima wake kwa ajili yake. Alifanya hivi kusudi atakase kanisa kwa ajili ya Mungu, akilisafisha kwa maji na kwa neno. Alitaka hivi kujipatia yeye mwenyewe kanisa tukufu na takatifu, lisilokuwa na taka wala kikunjo wala kilema chochote. Hivi vilevile waume wanapaswa kupenda wake wao kama vile wanavyopenda miili yao wenyewe. Yule anayependa muke wake, anajipenda yeye mwenyewe. Kwa maana hakuna mutu anayeweza kuchukia mwili wake mwenyewe, lakini anaukulisha na kuuchunga kama Kristo anavyotendea kanisa, kwa sababu sisi ni viungo vya mwili wake. Ni sawasawa inavyosemwa katika Maandiko Matakatifu: “Kwa sababu hii, mume ataacha baba yake na mama yake na kuungana na muke wake, nao wawili watakuwa mwili mumoja.” Ni vigumu sana kuelewa siri hii, lakini ninasema mambo yanayoelekea Kristo na kanisa. Ingawa hivi, kwa ngambo yenu vilevile, kila mume anapaswa kumupenda muke wake kama vile anavyojipenda, na kila muke anapaswa kuheshimu mume wake. Ninyi watoto muwatii wazazi wenu mbele ya Bwana, kwa maana vile ndivyo inavyostahili. “Heshimu baba yako na mama yako.” Hii ni amri ya kwanza ambayo waliongeza ahadi hii juu yake: “Kusudi upate heri na uishi siku nyingi katika dunia.” Na ninyi wababa musiwakasirikishe watoto wenu. Lakini muwalee na kuwaonya, mukiwatolea mashauri yanayotoka kwa Bwana. Ninyi watumwa, mutii wabwana wenu kwa woga na kutetemeka na kwa moyo wa ukweli kama vile munavyomutumikia Kristo. Musitumike tu wakati wanapowaangalia, mukitafuta kuwapendeza. Lakini mutimize mapenzi ya Mungu kwa moyo wote mukijihesabu kama watumwa wa Kristo. Mufanye kazi yenu ya utumwa kwa moyo mwema, kama vile wenye kumutumikia Bwana, wala si watu tu. Mukumbuke kwamba Bwana atalipa kila mutu sawa na matendo yake mema, akiwa huru au mutumwa. Na ninyi wabwana muwatendee watumwa wenu hivi vilevile. Muache kuwatisha, mukijua kwamba ninyi na watumwa wenu muko na Bwana mumoja mbinguni, naye hafanyi kitu kwa upendeleo. Basi kwa kumaliza, musimame imara katika kuungana kwenu na Bwana kwa uwezo wa nguvu zake kubwa. Muvae silaha zote Mungu anazowapa, kusudi mupate kushinda mayele ya Shetani. Kwa maana hatupigani na watu wa dunia hii, lakini tunapigana na pepo mbaya zinazokaa katika eneo la mbingu pamoja na wakubwa, na wenye mamlaka na watawala wa dunia hii ya giza. Kwa hiyo sasa mutwae silaha zote Mungu anazowapatia. Kwa njia hii mutaweza kushinda adui yenu siku mbaya itakapowafikia. Nanyi mutakapokwisha kumaliza mapigano, mutaweza kusimama imara. Basi, mujiweke tayari: mukijifungia ukweli kama vile mukaba, mukivaa haki kama vile nguo ya chuma ya kukingia kifua, na mukuwe na bidii ya kutangaza Habari Njema ya amani kama vile viatu munavyovaa. Na zaidi ya hivi vyote, muchunge imani kama vile munavyoshika ngao, kusudi mupate kuzimisha mishale yote yenye moto ya yule Mwovu. Mupokee wokovu kama vile kofia ya chuma ya kuwalinda, na Neno la Mungu kama upanga munaopewa na Roho. Mumwombe Mungu kila wakati mukiongozwa na Roho. Mumwombe na kumusihi kwa kila namna. Kwa hiyo mukeshe bila kuchoka mukiwaombea watu wote wa Mungu. Muniombee vilevile, kusudi Mungu anijalie maneno ya kusema. Kwa hiyo nitaweza kuwajulisha watu kwa uhodari siri ya Habari Njema. Mimi ni mujumbe wa Habari ile Njema, ijapokuwa sasa ninakuwa katika kifungo. Basi muniombee kusudi nipate kusema kwa uhodari, sawa inavyonipasa kusema. Tikiko, ndugu yetu mupendwa na mutumishi mwaminifu wa Bwana atawapasha habari zangu zote, kusudi mupate kujua kama mimi ni katika hali gani na namna kazi inavyoendelea. Ni kwa shabaha hiyo ninamutuma kwenu, apate kuwajulisha habari zetu na kuwafariji. Ninawatakia wandugu amani, upendo na imani kutoka kwa Mungu Baba na kwa Bwana Yesu Kristo. Ninawatakia neema wale wote wanaomupenda Bwana wetu Yesu Kristo kwa upendo usiokuwa na mwisho. Barua hii inatoka kwangu mimi Paulo na kwa ndugu yetu Timoteo, sisi watumishi wa Yesu Kristo. Tunawaandikia watu wote wa Mungu wanaoungana na Yesu Kristo, wanaoishi Filipi, pamoja na wazee wa kanisa na wasaidizi. Tunawatakia neema na amani toka kwa Mungu Baba yetu na kwa Bwana wetu Yesu Kristo. Ninamushukuru Mungu wangu kwa ajili yenu kila mara ninapowakumbuka. Kila wakati ninapowaombea ninyi, ninaomba kwa furaha, kwa namna munashirikiana nami katika kazi ya kutangaza Habari Njema, tangu mwanzo mpaka sasa. Ninajua hakika kwamba Mungu aliyeanza kazi hii njema ndani yenu, ataitimiza mpaka siku ile ya kurudi kwa Yesu Kristo. Ni haki kwangu kuwa na mafikiri haya kwa ajili yenu ninyi wote, kwa sababu ninawakumbuka kila mara. Kwa maana mumeshiriki pamoja nami katika neema ile Mungu aliyonipatia, ingawa sasa niko katika kifungo hata na wakati nilipokuwa huru kutetea na kuimarisha Habari Njema. Mungu ni mushuhuda wangu kwamba ninawapenda sana ninyi wote na moyo wa upendo mukubwa wa Yesu Kristo. Na kitu ninachoomba kwa Mungu, ni kwamba upendo wenu uzidi kuongezeka katika ufahamu wa kweli na usikilivu kamili, kusudi mupate kutambua mambo yanayokuwa bora zaidi. Kwa hivi mutakuwa safi pasipo kosa kwa Siku ile ya kurudia kwa Kristo. Maisha yenu yatajazwa matendo ya haki ambayo Yesu Kristo anayowajalia, kwa ajili ya utukufu na sifa ya Mungu. Wandugu zangu, ninataka mujue kwamba mambo yaliyonifikia yamesaidia kwa kuendelesha Habari Njema. Kutokana na hayo, walinzi wote wa nyumba ya mufalme pamoja na wengine wote, wanajua kwamba niko katika kifungo kwa sababu ninamutumikia Kristo. Kwa ajili ya kufungwa kwangu, wandugu wengi wamemwamini Bwana na kuwa na bidii sana ya kutangaza Neno la Mungu pasipo woga. Ni kweli kwamba wengi kati yao wanahubiri habari za Kristo kwa wivu na ugomvi, lakini wengine wanahubiri katika nia nzuri. Hawa wanahubiri kwa upendo, kwa maana wanajua kwamba Mungu amenipatia kazi ya kuitetea Habari Njema. Wale wengine wanatangaza habari za Kristo na roho ya mapingano na nia yao ni mbaya, wanafikiri kwamba wataniongezea mateso katika kifungo. Basi si kitu! Ikiwa nia yao ni mbaya au ni nzuri habari za Kristo zinatangazwa kwa namna mbalimbali, kwa hiyo ninafurahi. Na nitaendelea kufurahi tena, kwa maana ninajua kwamba kwa ajili ya maombi yenu na kwa musaada wa Roho wa Yesu Kristo nitakombolewa. Kwa maana kama vile ninavyongojea na kutumainia sana, sitafezeheka hata kidogo. Lakini tangia sasa na hata siku zote, nitamutukuza Kristo kwa uhodari katika maisha yangu, ikiwa nitaishi au nitakufa. Hivi kwangu kuishi ni kwa ajili ya Kristo na kufa ni faida. Lakini ikiwa kama kuendelea kuishi ni kwa lazima kwa ajili ya kazi yangu, basi sijui nichague nini. Maana ninasongwa na mambo mawili. Ninatamani kujiendea na kukaa pamoja na Kristo, maana hili ndilo jambo bora zaidi. Lakini jambo la lazima zaidi kwa ajili yenu, mimi niendelee kuishi. Basi niko na uhakika juu ya jambo hili nami ninajua kwamba nitabaki. Nitakaa pamoja nanyi kwa kuwasaidia kusudi mupate kuendelea na kuwa na furaha katika imani. Halafu, nitakaporudia tena kwenu, mutajivuna zaidi kwa ajili yangu katika kuungana kwenu na Yesu Kristo. Kitu cha lazima ni kwamba mukuwe na mwenendo unaolingana na mafundisho ya Habari Njema ya Kristo. Kwa hivi hata kama nikikuja kuwaona au hata kama nisipokuja, nipate tu kusikia kwamba munasimama imara katika nia moja, na kwamba wote pamoja munapigana vita kwa ajili ya imani inayotokana na Habari Njema. Musiogope waadui zenu hata kidogo. Hii itakuwa kitambulisho kwao kwa kuhakikisha kwamba wanapotea, lakini kwenu ni kwamba munaokolewa. Na hii inatoka kwa Mungu. Kwa maana Mungu amewapa ninyi neema ya kumutumikia Kristo, na si kwa kumwamini tu, lakini vilevile kwa kuteswa kwa ajili yake. Sasa munashiriki pamoja nami katika vita. Ninyi muliniona nikipigana vita ile na hata sasa munasikia kama ninapigana vita ile. Maisha yenu katika kuungana kwenu na Kristo si yanawatia ninyi nguvu? Nao upendo wake si unawafariji ninyi? Si munaishi katika ushirika na Roho Mutakatifu? Si muko na moyo mwema na wa huruma? Basi munijaze na furaha tele, mukiwa na nia moja, na upendo mumoja, roho moja na wazo moja. Musifanye jambo lolote kwa roho ya mapingano wala kwa kujivuna bure, lakini munyenyekeane kila mutu akimuhesabu mwenzake kuwa muzuri kuliko yeye mwenyewe. Kila mutu asitafute faida yake mwenyewe, lakini atafute faida ya watu wengine. Ndani yenu mukuwe na nia kama hii iliyokuwa ndani ya Kristo Yesu: Tangu mwanzo yeye alikuwa na hali ya Mungu, lakini hakuona kwamba kuwa sawa na Mungu ni kitu cha kushikamana nacho. Alitupilia hivi vyote, akatwaa hali ya mutumwa. Akatwaa mufano wa mutu, naye akaonekana katika hali ya kimutu. Alijinyenyekeza na kutii mpaka kufa, ndiko kufa kwake juu ya musalaba. Kwa hiyo Mungu naye akamwinua juu zaidi, akamupa jina lenye ukubwa kuliko majina yote, kusudi kwa kuheshimu jina la Yesu, viumbe vyote vinavyokuwa katika mbingu, katika dunia na katika kuzimu, vipige magoti mbele yake, na kila mutu akubali kwamba Yesu ni Bwana, naye Mungu Baba atatukuzwa kwa njia hiyo. Basi wapendwa wangu, mulionyesha utii wenu siku zote wakati nilipokuwa kwenu, na sasa ingekuwa vema muendelee kufanya vile katika siku hizi ninapokuwa mbali nanyi. Mutumike kwa ajili ya wokovu wenu kwa woga na kutetemeka, kwa maana Mungu anafanya kazi ndani yenu na kuwapa moyo wa kutaka na kutimiza mambo yanayolingana na mupango wake mwema. Mufanye kila kitu bila manunguniko wala mabishano, kusudi mupate kuwa bila kosa na kuwa na maisha safi. Hivi mutakuwa watoto wakamilifu wa Mungu wasiokuwa na kilema kati ya watu waovu na wapotovu wa dunia hii. Munapaswa kuangaza kati ya watu hawa kama vile nyota zinavyoangaza katika mbingu, mukiwatangazia habari inayoleta uzima. Hivi nitapata sababu ya kujivuna Siku ile ya kurudia kwa Kristo kwa maana itakuwa kitambulisho cha kuhakikisha kwamba bidii yangu na kazi yangu havikupotea bure. Hata nikitoa maisha yangu kuwa sadaka pamoja na imani yenu inayokuwa sadaka mbele ya Mungu, mimi ninafurahi na kushiriki pamoja nanyi wote. Nanyi vilevile mufurahi na kushiriki pamoja nami katika furaha yenu. Kama Bwana Yesu akitaka, ninangojea kisha muda kidogo kuwatumia Timoteo, kusudi nipate kutiwa moyo na habari nitakazopata kutoka kwenu. Ni yeye tu ndiye mafikiri yake yanapatana na yangu, naye anashugulika kweli na mambo yanayowaelekea. Watu wengine wote wanatafuta faida yao wenyewe, lakini hawashuguliki na Yesu Kristo. Munajua ninyi wenyewe namna Timoteo alivyojionyesha kwamba anastahili, kwa maana alitumika kazi ya kueleza Habari Njema pamoja nami kama vile mwana anavyotumika na baba yake. Ninatumaini kumutuma kwenu pale pale nitakapojua yale yatakayonitokea juu ya kufungwa kwangu. Nami ninamutumainia Bwana kwamba mimi mwenyewe nitakuja kuwaona bado kidogo. Niliona vema kuwatumia ndugu yetu Epafrodito, anayeshiriki pamoja nami katika kazi na katika vita ya Habari Njema. Ni yeye ndiye muliyetumia kwa kunisaidia kufuatana na mahitaji niliyokuwa nayo. Yeye yuko na hamu sana kuwaona ninyi wote, naye anahuzunika sana kwa sababu mulisikia kwamba alikuwa mugonjwa. Alikuwa mugonjwa karibu kufa, lakini Mungu akamuhurumia, na si yeye peke yake, lakini mimi vilevile kusudi nisikuwe na huzuni juu ya ingine. Hivi ninamutuma kwenu kwa haraka kusudi mupate kufurahi wakati mutakapomwona tena na huzuni yangu ipate kupunguka. Basi mumupokee kwa furaha kubwa sana kwa jina la Bwana. Munapaswa kuwapa watu wa namna hii heshima, kwa sababu yeye alikuwa karibu kufa kwa ajili ya kazi ya Kristo. Alihatarisha maisha yake kwa kuja kuniletea musaada ule ambao ninyi wenyewe musingeweza kunipatia. Kwa kumaliza, wandugu zangu, mufurahi kwa ajili ya kuungana kwenu na Bwana. Hainiuzi kitu kuwaandikia tena maneno yale yale niliyowaandikia mbele. Hayo yote ni kwa ajili ya kuwakingia hatari. Mufanye angalisho na watenda maovu, wale imbwa wanaotia mukazo juu ya kushika tu desturi ya kutahiriwa. Sisi ndio wenye kutahiriwa kwa kweli, maana tunamwabudu Mungu kwa uongozi wa Roho wake na kujivuna kwa ajili ya Yesu Kristo. Sisi hatuweki tumaini letu katika mambo ya kimwili. Lakini mimi vilevile niko na haki ya kuweka tumaini katika mambo ya kimwili. Kama kuna mutu anayejizania kuwa na sababu ya kutumainia mambo ya kimwili, mimi ninamupita. Nilitahiriwa nilipokuwa na umri wa siku nane. Mimi ni Mwisraeli, wa kabila la Benjamina, Mwebrania wa asili kabisa. Kuelekea mambo ya Sheria ya Kiyuda, nilikuwa Mufarisayo, nilikuwa na bidii sana hata nilitesa kanisa. Kuelekea mambo ya kuhesabiwa kwa njia ya kushika Sheria, mimi sikupatikana na kosa lo lote. Lakini mambo yote yaliyokuwa ya faida kwangu, sasa kwa ajili ya Kristo, ninayahesabu kama kihombo. Bila shaka, ninahesabu mambo yote kuwa kihombo kwa ajili ya faida kubwa ya kujua Kristo Yesu Bwana wangu. Kwa ajili yake nimekubali kupoteza vyote, nikivihesabu kuwa kama mavi, kusudi nimupate Kristo na kuungana naye kabisa. Nami sihesabiwi haki tena kufuatana na mambo niliyofanya, ndiyo ile haki inayopatikana kwa njia ya kushika Sheria. Lakini ninahesabiwa haki kwa njia ya kumwamini Kristo, ndiyo ile haki inatoka kwa Mungu, naye anamuhesabia haki yule anayeamini. Kitu ninachotaka tu, ni kumujua Kristo na uwezo wa ufufuko wake na kushirikiana naye katika mateso yake, nako kufa kwangu kufanane na kufa kwake. Nipate hivi tumaini kwamba nitafufuka vilevile. Sitaki kusema kwamba nimekwisha kufikia mwisho au kwamba nimekwisha kuwa mukamilifu. Lakini ninakaza mwendo kusudi nipate kushinda na kupokea zawadi, kwa maana Yesu Kristo amekwisha kunipokea nikuwe wake. Wandugu zangu, sihesabu kwamba nimekwisha kupokea zawadi, lakini ninafanya jambo moja tu: ninasahau yanayokuwa nyuma, nikifukuzia yanayokuwa mbele yangu. Kwa hiyo ninakaza mwendo mpaka mwisho nipate kupokea ile zawadi Mungu aliyotuitia katika mbingu kwa njia ya Yesu Kristo. Sisi wote tunaokomaa kiroho, tukuwe na shabaha hiyo moja. Na kukiwa wamoja katikati yenu wanaokuwa na mafikiri mbalimbali, Mungu atawafunulia maneno yale. Ingawa hayo yote, basi tuendelee mbele tokea kwenye hatua ile tumekwisha kufikia. Wandugu zangu, mufuate mufano wangu, muwaangalie vizuri wale wanaofuata mwenendo muliouona kwetu. Mimi nimewaambia mara nyingi, nami ninawaambia tena kwa machozi: kuna watu wengi wanaoonyesha kwa njia ya mwenendo wao kwamba kufa kwa Kristo juu ya musalaba ni chukizo kwao. Mwisho wao ni uharibifu, sababu mungu wao ni kushibisha tumbo zao. Wanajivuna kwa kufanya mambo ya kuwafezehesha. Nayo mafikiri yao ni juu ya vitu vya dunia hii. Lakini sisi ni wenyeji wa mbingu, tunamungojea Mwokozi wetu Bwana Yesu Kristo, afike kutoka kule. Yeye atabadilisha huu mwili wetu wa uzaifu na kuufananisha na mwili wake wa utukufu kwa nguvu ambayo kwa njia yake anaweza kuwa na mamlaka juu ya vitu vyote. Kwa hiyo wandugu zangu wapendwa, niko na hamu sana ya kuwaona tena. Ninyi ndio munaokuwa furaha yangu na zawadi ya ushindi nitakayopokea. Ninyi wapendwa wangu, ninawaomba musimame imara katika ushirika wenu na Bwana. Ninakusihi wewe Ewodia na wewe Sintike, muishi katika masikilizano mbele ya Bwana. Na wewe vilevile mutumishi mwenzangu mwaminifu, ninakuomba uwasaidie wanawake hao, kwa maana walisumbuka sana pamoja nami katika kazi ya kutangaza Habari Njema. Kuko vilevile Klementi na wenzangu wengine wa kazi. Hao wote majina yao yameandikwa katika kitabu cha uzima. Mufurahi siku zote katika kuungana kwenu na Bwana. Na tena ninasema: Mufurahi! Muonyeshe upole wenu kwa watu wote, kwa maana Bwana yuko karibu kurudia. Musijisumbue juu ya neno lolote, lakini katika kila neno mutoe mahitaji yenu kwa Mungu, mukimwomba, mukimusihi na kumushukuru. Na amani ya Mungu inayopita ufahamu wa mutu yeyote, italinda mioyo yenu na nia zenu salama katika kuungana kwenu na Yesu Kristo. Kwa kumaliza, wandugu zangu, muweke mafikiri yenu juu ya mambo yote yanayokuwa ya kweli, ya heshima, ya haki, safi, ya kupendeza, nayo mambo yote yanayostahili sifa na ya utu wema. Mushike mambo yote muliyojifunza na kupokea toka kwangu, nayo yote muliyosikia na kuona kwangu. Naye Mungu wa amani atakuwa pamoja nanyi. Nilipata furaha kubwa katika kuungana na Bwana kwa kuona munakumbuka tena kunisaidia. Sitaki kusema kwamba mulinisahau, lakini hamukupata wakati wa kuonyesha kwamba munanishugulikia. Na sisemi hivi kwa sababu ninakosewa na kitu, kwa maana ninajizoeza kufurahi na kile ninachokuwa nacho. Ninajua kuishi katika ukosefu na ninajua kuishi katika utajiri. Nimejizoeza kufurahi fasi zote na katika kila hali: ikiwa hali ya kuwa na vyakula kwa uwingi au ya njaa, ikiwa hali ya utajiri au ya ukosefu. Ninaweza vyote kwa njia ya Kristo anayenitia nguvu. Lakini, mumefanya vizuri kwa kushirikiana pamoja nami katika taabu yangu. Ninyi Wafilipi munajua vizuri wenyewe kwamba nilipotoka Makedonia, tangu mwanzo wa kuhubiri Habari Njema, ni ninyi tu ndilo kanisa moja lililoshirikiana nami katika mambo ya utoaji na upokeaji. Hata wakati wote nilipokuwa Tesalonika, mulinitumia musaada mara nyingi juu ya mahitaji yangu. Sitaki kusema kwamba ninatafuta tu kupokea zawadi, lakini ninataka faida iongezwe kwa upande wenu. Kweli nina vitu vyote vya lazima na zaidi kupita. Sasa kwa kuwa Epafrodito ameniletea zawadi zenu zote, ninatosheka. Zawadi hizi ni kama sadaka ya ubani yenye harufu nzuri, na kama sadaka ya kuteketezwa kwa moto inayokubaliwa na Mungu na kumupendeza. Basi, kwa njia ya Yesu Kristo, Mungu wangu atatimiza mahitaji yenu yote kufuatana na uwingi na utukufu wa utajiri wake. Mungu Baba yetu atukuzwe kwa milele na milele. Amina. Musalimie watu wote wa Mungu wanaomwamini Yesu Kristo. Wandugu wanaokuwa pamoja nami wanawasalimia. Watu wote wa Mungu, na hasa zaidi wale wanaokuwa katika nyumba ya Mufalme, wanawasalimia vilevile. Ninawatakia ninyi wote neema kutoka kwa Bwana wetu Yesu Kristo. Barua hii inatoka kwangu mimi Paulo na kwa ndugu yetu Timoteo. Mimi niliitwa na Mungu kwa mapenzi yake kuwa mutume wa Yesu Kristo. Tunawaandikia ninyi watu wa Mungu munaokaa katika muji Kolosayi, ninyi wandugu munaoungana na Kristo kwa uaminifu. Tunawatakia neema na amani toka kwa Mungu Baba yetu. Tunamushukuru Mungu, Baba ya Bwana wetu Yesu Kristo kila mara tunapowaombea ninyi. Hayo yote ni kwa maana tumesikia namna munavyomwamini Yesu Kristo na namna munavyowapenda watu wote wa Mungu. Imani yenu na upendo wenu vinakuwa na musingi katika tumaini mulilowekewa mbinguni. Mulisikia juu ya tumaini lile mara ya kwanza wakati mulipohubiriwa ujumbe wa ukweli ni kusema Habari Njema. Habari Njema ile inatoa matunda na kuenea katika dunia yote sawa vile ilivyofanya kwenu tangu siku ile muliposikia wakisema juu ya neema ya Mungu na kupata kuitambua inavyokuwa kweli. Ni Epafra mutumishi mwenzetu mupenzi, ndiye aliyewafundisha ninyi habari zile. Yeye ni mutumishi mwaminifu wa Kristo kwa ajili yetu. Yeye ndiye aliyetupatia habari za upendo wenu muliojaliwa na Roho. Kwa sababu hii hatuchoki kuwaombea ninyi, tangu siku tuliposikia habari zenu. Tunamwomba Mungu awawezeshe kujua kabisa mapenzi yake na kuwajaza hekima na akili inayotoka kwa Roho wake. Hivi, mutaweza kuishi sawa Bwana anavyotaka na kumupendeza katika mambo yote. Kwa njia hiyo mutafikia kufanya matendo mema ya kila namna na kuzidi kumujua Mungu. Mungu atawatia nguvu kwa uwezo wake wenye utukufu, kusudi mupate kuvumilia kila kitu pasipo kuchoka. Basi kwa furaha, mumushukuru Mungu Baba aliyewawezesha ninyi kuwa wenye kustahili kupokea sehemu yenu ya urizi aliowawekea watu wake katika ufalme wa mwangaza. Kwa maana yeye ametuokoa toka katika uwezo wa giza, na kutuingiza katika ufalme wa Mwana wake mupendwa, ambaye katika yeye tumekombolewa na kusamehewa zambi zetu. Kristo ni mufano kamili wa Mungu asiyeonekana. Yeye ni muzaliwa wa kwanza wa viumbe vyote. Kwa njia yake, Mungu aliumba vitu vyote vinavyokuwa mbinguni na katika dunia, vyenye kuonekana na visivyoonekana; ikiwa ni ufalme, ukubwa, utawala au mamlaka. Mungu aliumba vyote kwa njia yake na kwa ajili yake. Kristo alikuwa yuko mbele vitu vyote havijakuwa, na kwa njia ya kuungana naye vyote vinashikamana. Yeye ni kichwa cha kanisa linalokuwa mwili wake. Naye ndiye asili ya uzima wa mwili ule. Yeye ndiye mwanzo, muzaliwa wa kwanza, na ndiye aliyefufuka wa kwanza, kusudi akuwe wa kwanza juu ya vyote. Kwa maana Mungu mwenyewe alitaka ukamilifu wake uonekane ndani ya mwana wake. Kwa njia ya Mwana wake alitaka kupatanisha ulimwengu muzima naye. Kwa njia ya damu ya Mwana wake iliyomwangika juu ya musalaba, Mungu ameleta amani, hivi akapatanisha vitu vyote naye mwenyewe, vinavyokuwa katika dunia na katika mbingu. Na ninyi zamani mulikuwa mbali na Mungu, mulikuwa waadui zake kwa sababu ya mafikiri na matendo yenu mabaya. Sasa, Mungu amewapatanisha ninyi naye, kwa njia ya kufa kwa Mwana wake kimwili, kusudi awawezeshe kuonekana mbele yake mukiwa watakatifu, bila kilema wala kosa lolote. Lakini, inawapasa ninyi kuendelea na musingi imara katika imani, musitikiswe na kupoteza lile tumaini mulilopata wakati muliposikia Habari Njema. Mimi Paulo nimewekwa kuwa mutumishi wa kuhubiri Habari Njema ile iliyokwisha kutangazwa kwa watu wote katika dunia. Sasa ninafurahi kwa ajili ya mateso ninayopata juu yenu. Kwa njia ya kuteseka kwangu kimwili, ninatimiza mateso yaliyomubakilia Kristo kwa ajili ya mwili wake, maana yake kanisa. Mimi nimekuwa mutumishi wa kanisa kufuatana na kazi ile Mungu aliyonipa kwa ajili yenu. Kazi yenyewe ni kutangaza Neno lake kwa ukamilifu. Neno lile ndio ile siri aliyoificha tangu zamani za kale, lakini sasa ameifunua kwa watu wake. Kwa maana Mungu alitaka kuwafunulia watu hao siri ya mupango wake wenye utajiri mukubwa alioufanya kwa ajili ya mataifa yote. Nayo siri ile ni kwamba Kristo ni ndani yenu, naye ndiye anayetuletea tumaini kwamba tutashiriki katika utukufu wa Mungu. Ni kwa hiyo tunamutangaza Kristo kwa watu wote. Tunaonya na kufundisha kila mutu kwa hekima yote, kusudi tuwasaidie watu wote wapate kufikia kuwa wakamilifu katika kuungana kwao na Kristo. Ni kwa sababu hiyo ninatumika na kupigana kwa uwezo ninaopewa na Kristo, unaoniwezesha kufanya kazi kwa nguvu. Ninataka mujue jinsi ninavyofanya kazi kwa bidii kwa ajili yenu, kwa ajili ya waamini wa Laodikia na kwa ajili ya wote ambao hawajapata kuniona bado. Ninapigana kusudi wapate kuwa na bidii na kuungana katika upendo. Na zaidi ya hii wapate kuwa na uhakika kabisa unaotokana na ufahamu mukamilifu. Hivi wataweza kujua siri ya Mungu, maana yake kumujua Kristo mwenyewe, kwa maana hazina zote za hekima na elimu zimefichwa ndani yake. Ninawaambia ninyi maneno haya kusudi mutu asiwadanganye kwa maneno matamu ya kupotosha. Ijapokuwa mimi ni mbali nanyi kwa mwili, lakini mimi ni pamoja nanyi kwa roho, nami ninafurahi kuona namna munavyoishi katika utaratibu muzuri na kusimama imara katika imani mbele ya Kristo. Basi kwa sababu mumemukubali Kristo kuwa Bwana wenu, muishi katika kuungana naye. Mukuwe na mizizi ndani yake, mujijenge juu yake na kusimama imara katika imani sawa vile mulivyofundishwa. Na zaidi ya hii mukuwe wenye kushukuru sana. Mujiangalie hata mutu asiwapotoshe kwa elimu yake ya udanganyifu mutupu inayotegemea desturi za watu na roho mbaya zinazotawala dunia, lakini haitegemei mafundisho ya Kristo. Kwa maana ukamilifu wote wa Mungu uko ndani ya Kristo katika mwili wake. Na kwa kuungana naye, ninyi mumepata kukamilika. Yeye ndiye anayetawala roho zote zenye mamlaka na uwezo. Katika kuungana naye, mumetahiriwa wala si kwa mikono ya watu, lakini mumetahiriwa na Kristo, na kutahiriwa kule kumewakomboa toka katika hali zaifu ya kimwili. Kwa maana mumezikwa pamoja na Kristo kwa njia ya ubatizo, nanyi mumefufuliwa vilevile pamoja naye, kwa sababu mumeamini uwezo wa Mungu, aliyemufufua. Zamani mulikuwa mumekufa kwa sababu ya zambi zenu na kwa sababu mulikuwa watu wa mataifa mengine, wasiotahiriwa. Lakini sasa, Mungu amewapatia ninyi uzima pamoja na Kristo, naye ametusamehe zambi zetu zote. Alifuta barua ya madeni yetu na sherti zilizotushitaki. Aliyafuta kabisa kwa kuyapigilia juu ya musalaba. Mungu alinyanganya uwezo wa wakubwa na wenye mamlaka, naye akawaonyesha waziwazi, akiwatembeza kama wafungwa katika maandamano ya ushindi wa Mwana wake. Basi, mutu asiwahukumu juu ya chakula au kinywaji, au juu ya kushika sikukuu fulani, ikiwa sikukuu ya Mwandamo wa Mwezi au siku ya Sabato. Mambo hayo yote ni kivuli cha mambo yatakayokuja, lakini ukweli wa mambo yote ni Kristo mwenyewe. Musikubali kuhukumiwa na mutu yeyote anayejionyesha kwa inje kuwa yeye ni munyenyekevu na mwenye kuabudu malaika. Mutu wa namna hii anatia sana maana juu ya maono anayopata, naye anajitapa bure juu ya mafikiri yake ya kimutu. Mutu yule hashikamani na Kristo anayekuwa kichwa cha mwili. Chini ya uongozi wa Kristo, mwili muzima unakulishwa vizuri na kuunganishwa pamoja kwa njia ya maunganio na vifundo vyake, kusudi upate kukomaa kufuatana na mapenzi ya Mungu. Ninyi mumekufa pamoja na Kristo na kukombolewa toka katika uwezo wa roho mbaya zinazotawala dunia. Kwa nini munaishi tena kama watu wa dunia mukilazimishwa kushika kanuni kama hizi: “Usikule hiki”, “Usionje hiki,” “Usiguse hiki na hiki!” Mambo hayo yote yanaelekea vitu vyenye kuharibika mara moja tu vinapotumiwa. Navyo vyote ni kanuni na mafundisho ya watu tu. Hakika kanuni hizi zinaonekana kama za hekima kwa maana zinatokana na ibada ya kipekee ya watu wale pamoja na unyenyekevu wao na shurti zao za kuutesa mwili. Lakini hazifai kitu kwa kuzuiza tamaa za mwili. Kwa kuwa mumefufuliwa pamoja na Kristo, mutafute mambo yanayokuwa juu, pahali Kristo anapoikaa na mamlaka kwa kuume kwa Mungu. Mushugulikie sana mambo yanayokuwa juu, lakini musishugulikie mambo yanayokuwa katika dunia. Kwa maana ninyi mumekufa na uzima wenu umefichwa pamoja na Kristo katika Mungu. Kristo ndiye uzima wenu wa kweli, naye atakapoonekana tena, basi ninyi mutaonekana pamoja naye katika utukufu wake. Basi mutupilie mbali mambo yote ya kidunia yanayokuwa ndani yenu: uasherati, uchafu, nia mbaya, tamaa mbaya na tamaa ya mali inayokuwa sawa vile kuabudu sanamu. Kwa sababu ya makosa haya, kasirani ya Mungu itawaangukia wale wanaomwasi. Zamani, ninyi muliishi kwa namna ile mulipokuwa mukitawaliwa na mambo hayo ya zambi. Lakini sasa mutupilie mbali mambo haya yote: kasirani, chuki, uovu, masingiziano na musiseme neno lolote baya. Musiambiane uongo ninyi kwa ninyi, kwa maana mumeondoa utu wenu wa zamani pamoja na matendo yake na kuvaa utu mupya. Utu ule unaendelea kufanywa upya kila mara kufuatana na mufano wa Mungu anayekuwa muumba wake, kusudi mupate kumujua hakika. Kwa hiyo hakuna tena tofauti kati ya watu wa mataifa mengine na Wayuda, wenye kutahiriwa na wasiotahiriwa, wageni, washenzi, watumwa na watu huru. Lakini Kristo ni yote naye yuko katika wote. Ninyi ni watu wa Mungu, yeye amewapenda na kuwachagua kwa ajili yake mwenyewe. Kwa hiyo, mukuwe na moyo wa huruma, wema, unyenyekevu, upole na uvumilivu. Muvumiliane na kusameheana ninyi kwa ninyi wakati wowote mutu anapokuwa na neno la kumushitaki mwingine. Munapaswa kusameheana kama vile Bwana alivyowasamehe ninyi. Zaidi ya mambo haya yote, mukuwe na upendo, maana upendo unaunganisha kila kitu katika umoja unaokuwa mukamilifu. Amani ya Kristo itawale katika mioyo yenu; maana ni kwa ajili ya hiyo ninyi mumeitwa kuwa katika mwili mumoja. Mukuwe wenye shukrani. Habari za Kristo zikae ndani yenu kwa uwingi. Mufundishane na mushauriane kwa hekima. Mumwimbie Mungu kwa moyo wenu wote na kumushukuru kwa zaburi na nyimbo za kiroho. Kila kitu munachofanya au kusema, mufanye yote kwa jina la Bwana Yesu, kwa kumushukuru Mungu Baba kwa njia yake. Wake muwatii waume wenu kama vile inavyostahili mbele ya Bwana. Waume muwapende wake wenu nanyi musiwatendee kwa ukali. Watoto muwatii wazazi wenu katika mambo yote, kwa maana jambo hili linamupendeza Bwana. Ninyi wababa musiwakasirikishe watoto wenu, kusudi musiwavunje moyo. Ninyi watumwa, muwatii wabwana wenu katika mambo yote hapa katika dunia. Musiwatii tu wakati wanapowaangalia ninyi kama mungetaka tu kujipendeza mbele yao, lakini muwatii kwa moyo mwema, kwa sababu munamuheshimu Bwana. Na kila kitu munachofanya, mukifanye kwa moyo wenu wote, kama vile wenye kumutumikia Bwana wala si watu. Mukumbuke kwamba Bwana atawapa ninyi zawadi ile anayowawekea watu wake. Kwa maana Kristo ndiye Bwana wa kweli munayemutumikia. Lakini yule anayefanya mabaya, atalipwa kufuatana na mabaya aliyotenda, kwa sababu Mungu hana upendeleo. Ninyi wabwana muwatendee watumishi wenu kwa usawa na kwa haki, mukijua kwamba ninyi vilevile muko na Bwana wenu katika mbingu. Mudumu katika kuomba. Munapoomba mukeshe na kumutolea Mungu shukrani. Mutuombee sisi vilevile kusudi Mungu atufungulie njia ya kuhubiri neno lake tupate kutangaza ujumbe wa siri juu ya Kristo. Ni kwa ajili ya ujumbe ule mimi niko sasa katika kifungo. Basi muniombee kusudi nipate kuupasha waziwazi sawa ninavyopaswa kufanya. Mukuwe na mwenendo wa hekima mbele ya watu wanaokuwa wa inje ya kanisa, mukitumia vema kila wakati munaoupata. Masemi yenu yanapaswa kuwa mazuri siku zote na yenye kufaa, munapaswa kujua kujibia kila mutu vizuri. Ndugu yetu mupendwa Tikiko mutumishi mwaminifu, na mwenzangu tunayetumika naye kazi ya Bwana atawapasha ninyi habari zangu zote. Ni kwa shabaha hiyo ninamutuma kwenu apate kuwajulisha habari zetu na kuwafariji. Ninamutuma pamoja na ndugu mupendwa na mwaminifu, Onesimo, anayekuwa mwanainchi wa kule kwenu. Wao ndio watawaelezea maneno yote yaliyotokea hapa. Mufungwa mwenzangu Aristarko anawasalimia. Naye Marko, binamu wa Barnaba anawasalimia vilevile. (Mumekwisha kupata maagizo juu ya Marko; akifika kwenu mumupokee vizuri). Naye Yesu anayeitwa Yusto, anawasalimia ninyi vilevile. Kati ya Wayuda walioamini ni hao watatu tu ndio wanaotumika pamoja nami kwa ajili ya kazi inayoelekea Ufalme wa Mungu, nao wamenifariji sana. Mwanainchi mwenzenu Epafra anawasalimia vilevile. Yeye ni mutumishi wa Yesu Kristo, hachoki kwa kuwaombea ninyi, kusudi musimame imara mukikomaa kiroho na kuwa tayari kwa kutimiza kabisa mapenzi ya Mungu. Ninaweza kushuhudia juu yake kwamba anajisumbua sana kwa ajili yenu na kwa ajili ya wandugu wa Laodikia na wa Hierapoli. Luka, muganga wetu mupendwa na Dema wanawasalimia. Muwasalimie wandugu wa Laodikia, pamoja na Nimfa na kanisa linalokusanyika ndani ya nyumba yake. Barua hii itakapokwisha kusomwa kwenu mufanye namna yote ipate kusomwa vilevile katika kanisa la Laodikia. Na ninyi kwa ngambo yenu, musome vilevile barua niliyotuma kwa kanisa lile. Mumwambie Arkipo aangalie vizuri atimize kazi ile aliyopewa na Bwana. Mimi Paulo ninawatumia salamu zangu, nikiziandika kwa mukono wangu mwenyewe. Musisahau kwamba mimi ningali katika kifungo. Ninawatakia neema kutoka kwa Mungu. Barua hii inatoka kwangu mimi Paulo na kwa Silvano na Timoteo. Tunawaandikia ninyi kanisa la Tesalonika munaoungana na Mungu Baba na Bwana wetu Yesu Kristo. Tunawatakia neema na amani. Tunamushukuru Mungu siku zote kwa ajili yenu ninyi wote. Nasi tunawakumbuka katika maombi yetu bila kuchoka. Kwa maana tunakumbuka mbele ya Mungu Baba yetu namna munavyotumika kwa imani na munavyojisumbua na kazi kwa ajili ya upendo wenu. Vilevile tunakumbuka namna tumaini lenu katika Yesu Kristo linavyokuwa imara. Wandugu wapendwa wa Mungu, tunajua kwamba yeye amewachagua kuwa watu wake. Kwa maana tulipohubiri Habari Njema kwenu, hatukuihubiri kwa maneno tu, lakini kwa uwezo na kwa musaada wa Roho Mutakatifu na kwa uhakika kabisa. Munajua namna gani tulivyoishi katikati yenu, kusudi tupate kuwafalia. Ninyi mumefuata mufano wetu na mufano wa Bwana, kwa kuwa ingawa muliteswa sana, mulipokea neno la Mungu kwa furaha inayotoka kwa Roho Mutakatifu. Kwa njia hii mumeonyesha mufano muzuri kwa waamini wote wa Makedonia na Akaya. Kwa maana tokea kwenu neno la Bwana lilienea, si katika Makedonia na Akaya tu, lakini habari za imani kwa Mungu zilisambaa fasi zote, hata sisi hatukukuwa tena na lazima ya kusema neno juu ya ile. Wao wenyewe wanaeleza namna mulivyotupokea wakati tulipofika kwenu na namna mulivyoacha kuabudu sanamu na kumurudilia Mungu. Mulifanya vile kusudi mumutumikie Mungu mwenye uzima na wa kweli na kungojea Mwana wake Yesu kutoka mbinguni. Ni yule Mungu aliyemufufua, naye ndiye anayetuokoa toka kasirani ya hukumu ya Mungu inayokuja. Wandugu, munajua ninyi wenyewe kwamba safari yetu kwenu haikukuwa bure. Kama vile munavyojua, mbele ya kufika kwenu tuliteswa na kutukaniwa kwanza katika muji Filipi. Lakini ingawa tulipata vizuizo vingi, Mungu alitupatia uhodari wa kuwapasha ninyi Habari yake Njema. Mahubiri yetu si ya uongo, wala yenye nia mbaya wala ya udanganyifu. Lakini siku zote tunasema vile Mungu anavyotaka, kwa maana yeye aliamua kwamba tunastahili, akatupatia kazi ya kuhubiri Habari Njema yake. Sisi hatutafuti kuwapendeza watu, lakini tunataka kupendeza Mungu, anayejua siri za mioyo yetu. Kama vile munavyojua, hata siku moja hatukutumia masemi ya kujipendekeza kwa watu wala hatukutamani kupata mali kwa uficho; Mungu ni mushuhuda wetu. Hatukutafuta sifa ya watu wala yenu, wala ya mutu mwingine yeyote, ijapokuwa sisi ni mitume wa Kristo, tungeweza kudai mambo fulani kwenu. Lakini sisi tulionyesha upole kati yenu kama vile mama anavyosumbuka kwa ajili ya watoto wake. Sisi tunawapenda sana hata tumekuwa tayari, si kuwatolea Habari Njema ya Mungu tu, lakini kutoa maisha yetu kwa ajili yenu vilevile. Ni vile kwa sababu ninyi mumekuwa kweli wapendwa wetu. Wandugu, munakumbuka namna tulivyosumbuka na kazi ngumu. Wakati tulipowahubiria Habari Njema ya Mungu, tulitumika muchana na usiku kusudi tusimulemee hata mutu mumoja kati yenu. Ninyi ni washuhuda wetu, na Mungu vilevile anashuhudia kwamba tulipokaa kati yenu ninyi waamini, tuliishi katika utakatifu na haki, na bila kosa. Munajua vizuri kwamba tulimutendea kila mumoja wenu kama vile baba anavyowatendea watoto wake mwenyewe. Sisi tuliwaonya, tuliwafariji na kuwasihi sana muishi sawa inavyomupendeza Mungu, anayewaalika kushiriki naye katika ufalme na utukufu wake. Inatupasa tena kumushukuru Mungu siku zote kwa ajili ya jambo hili: muliposikia neno la Mungu kutoka kwetu, hamukulikubali kama vile neno la mutu, lakini kama vile kweli ndilo neno la Mungu. Na neno lile ndilo linalofanya kazi ndani ya mioyo yenu ninyi wanaoamini. Wandugu, mambo yale yale yaliyotokea makanisa ya Mungu ya Yudea yanayoungana na Yesu Kristo, ndiyo yaliyowatokea ninyi vilevile. Kwa maana ninyi muliteswa na wanainchi wenzenu kama vile wao walivyoteswa na wanainchi wenzao Wayuda. Ndio wale waliomwua Bwana Yesu na manabii, wakatutesa sisi vilevile. Wao hawamupendezi Mungu, nao ni waadui za watu wote! Wanajikaza kutuzuiza tusitangaze Habari Njema kwa watu wa mataifa mengine kusudi wasiokoke. Hivi wanafikilia kwenye hatua ya mwisho ya zambi walizotenda siku zote. Lakini kwa mwisho kasirani ya Mungu imewaangukia. Wandugu, sisi kwa ngambo yetu, tuliachana nanyi kwa muda kimwili, lakini si kiroho. Nyuma ya pale tulifanya bidii sana kusudi tuwafikie. Tulitaka kuja kule kwenu, zaidi sana mimi Paulo nilijaribu kufunga safari mara moja au mara mbili hivi, lakini Shetani alituzuiza. Ninyi peke yenu tu ndio tumaini, furaha, na taji ya ushindi tutakavyojivunia wakati Bwana Yesu Kristo atakaporudia. Kweli, ni kwa ajili yenu sisi tunajivuna na kufurahi. Kwa mwisho hatukuweza kuvumilia tena. Basi, tuliona vema kubaki Atene peke yetu na kumutuma ndugu yetu Timoteo, anayemutumikia Mungu pamoja nasi katika kazi ya kutangaza Habari Njema ya Kristo. Tulimutuma kwenu apate kuwatia nguvu na kuwafariji katika imani yenu, kusudi hata mumoja wenu asitikiswe na mateso haya tunayopata. Ninyi wenyewe munajua vema kwamba mateso kama hayo yalipaswa kututokea. Kwa maana wakati tulipokuwa pamoja nanyi, tulikuwa tumekwisha kuwaambia mbele ya wakati kwamba tutapata mateso. Na ni vile ilivyotutokea kama munavyojua. Ni kwa sababu hiyo, nilipoona kwamba siwezi kuendelea kungojea, nilimutuma Timoteo kusudi nipate kujua habari ya imani yenu. Niliogopa kwamba labda yule mushawishi Shetani amejaribu kuwaangusha ninyi na kwamba kazi yote tuliyofanya kwenu imepotea bure. Lakini sasa Timoteo amefika kwetu, akirudia toka kule kwenu. Ametuletea habari nzuri juu ya imani yenu na upendo wenu. Ametuelezea kwamba munatukumbuka vizuri siku zote, na kwamba muko na hamu sana ya kutuona, kama vile sisi nasi tunavyokuwa na hamu ya kuwaona. Kwa hiyo wandugu, katika taabu na mateso tunayopata, tumefarijiwa nanyi kwa kusikia habari za imani yenu. Kwa maana sasa tunaweza kupumua kwa kuona munasimama imara katika kuungana kwenu na Bwana. Sijui namna gani tunavyoweza kumushukuru Mungu kwa ajili yenu kwa sababu ya furaha yote tunayokuwa nayo mbele yake kwa ajili yenu. Usiku na muchana tunamwomba Mungu kwa bidii sana kusudi atupatie njia ya kuweza kuwaona tena na kuwaongezea kile munachokosewa katika imani yenu. Basi Mungu mwenyewe, Baba yetu, na Bwana wetu Yesu, watufungulie njia tupate kufika kwenu. Na Bwana awaongezee na kuwazidishia upendo munaokuwa nao ninyi kwa ninyi na kwa watu wote, kama vile sisi nasi tunavyowapenda ninyi. Vilevile aitie mioyo yenu nguvu nanyi mutapata kuwa watakatifu na bila kosa mbele ya Mungu Baba yetu siku Bwana wetu Yesu atakaporudia pamoja na watakatifu wake wote. Kwa mwisho, wandugu, sisi tumewafundisha namna gani munavyopaswa kuishi kusudi mupate kumupendeza Mungu. Na kweli, ni vile munavyoishi. Na sasa, tunawaomba na kuwasihi kwa jina la Bwana Yesu, muendelee mbele vizuri zaidi katika mwenendo ule. Kwa maana munajua maagizo gani tuliyowatolea kutoka kwa Bwana Yesu. Kitu Mungu anachotaka ni kwamba mukuwe watakatifu na muepuke mambo ya uasherati. Kila mwanaume anapaswa kujua namna ya kuishi na muke wake katika hali ya utakatifu na ya heshima, bila kujiachilia kutawaliwa na tamaa mbaya kama vile wapagani wasioamini Mungu. Kuelekea maneno hayo, mutu yeyote asimukosee ndugu yake wala kumudanganya. Tumekwisha kuwaambia na kuwahakikishia mbele kwamba Bwana atawaazibu wale wanaofanya mambo kama hayo. Kwa maana Mungu hakutuita kusudi tuishi katika uchafu, lakini katika utakatifu. Basi kwa hiyo, yeye anayekataa mafundisho haya hamukatai mutu, lakini anamukataa Mungu anayewapa ninyi Roho wake Mutakatifu. Na kuelekea upendo wa wandugu waamini, si lazima kwenu kuwaandikia neno lolote, kwa maana Mungu yeye mwenyewe amewafundisha ninyi kupendana. Ni vile mulivyojionyesha mbele ya wandugu wote wa kanisa la Makedonia. Na sasa tunawasihi ninyi wandugu, muendelee mbele vizuri zaidi katika jambo lile. Mufanye bidii sana mupate kuishi katika amani. Mushugulike na mambo yenu ninyi wenyewe na kufanya kazi kwa mikono yenu wenyewe sawa vile tulivyokwisha kuwaagiza. Hivi mutakuwa na mwenendo wa heshima mbele ya watu wasiokuwa wa Kristo, wala hamutahitaji kusaidiwa na mutu yeyote. Wandugu, hatutaki mukose kujua habari zinazowaelekea wale waliokufa, kusudi musikuwe na huzuni sawa vile watu wasiokuwa na tumaini la kufufuka. Tunaamini kwamba Yesu alikufa na alifufuliwa, na kwa hiyo tunaamini vilevile kwamba Mungu atawafufua pamoja na Yesu wale waliokufa wakimwamini Yesu. Kwa maana, kufuatana na mafundisho ya Bwana, tunawaambia hivi: sisi tutakaokutiwa wazima wakati Bwana atakaporudia, hatutawatangulia wale waliokufa. Kwa sababu amri itakapotoka na sauti ya malaika mukubwa itakaposikilika, na baragumu ya Mungu itakapolia, Bwana mwenyewe atashuka toka mbinguni. Halafu wale waliokufa wakimwamini Kristo watafufuliwa kwanza. Na kisha sisi tutakaokutiwa wazima wakati ule, tutanyanyuliwa pamoja nao katika mawingu kwa kukutana na Bwana katika anga. Na hivi tutakaa siku zote pamoja na Bwana. Basi ninyi mufarijiane kwa maneno haya. Wandugu, si lazima kwenu niwaandikie jambo lolote juu ya wakati wala saa ambayo mambo hayo yatatokea. Kwa maana munajua ninyi wenyewe kwamba siku Bwana atakaporudia, itatimia kwa saa musiyozania kama vile mwizi anavyokuja usiku. Watu watakapokuwa wakisema: “Kuna amani na usalama”, ndio wakati uharibifu utakapowapata kwa rafla kama vile maumivu ya kuzaa yanavyomupata mwanamuke mwenye mimba, wala hawataweza kuponyoka. Lakini ninyi wandugu, hamuko katika giza, kwa hiyo siku ile haitawafikia kwa rafla kama mwizi. Kwa maana ninyi wote ni watu wanaoishi katika mwangaza, ndio watu wa muchana. Sisi si watu wa usiku wala wa giza. Basi tusilale usingizi kama vile wengine, lakini tukeshe na kuwa wakadirifu. Kwa maana wale wanaolala usingizi wanalala usiku, na wale wanaolewa, wanalewa usiku. Lakini sisi ni watu wa muchana, tunapaswa kuwa wakadirifu. Tunapaswa kushikamana na imani na upendo kama vile nguo ya chuma ya kukingia kifua, nalo tumaini letu la wokovu kama vile kofia ya kutulinda. Kwa maana Mungu hakututayarishia kuangamizwa kwa ukali wa kasirani yake, lakini kuokolewa kwa njia ya Bwana wetu Yesu Kristo. Yeye alikufa kwa ajili yetu, kusudi hata ikiwa tuko wazima au tumekufa, tupate kuishi pamoja naye wakati atakaporudia. Basi mufarijiane na kujengana imani, kama vile munavyozoea kufanya. Wandugu, tunawaomba muwaheshimu sana wale wanaoshugulika na kazi kati yenu, wale wanaowaongoza na kuwaonya. Muwape heshima kubwa na kuwapenda kwa ajili ya kazi yao. Mukuwe na amani kati yenu. Tunawasihi wandugu, muwaonye wale wanaokuwa wavivu, muwatie moyo wale wanaoregea, muwasaidie wale wanaokuwa zaifu, na mukuwe wavumilivu kwa watu wote. Muangalie vema, hata mumoja wenu asimurudishie mwenzake ubaya kwa ubaya, lakini mutafutiane wema ninyi kwa ninyi na kwa watu wote. Mukuwe na furaha siku zote. Muombe bila kuchoka. Mumushukuru Mungu katika mambo yote. Kwa maana hayo ndiyo mambo Mungu anayotaka mufanye katika kuungana kwenu na Yesu Kristo. Musizuize kazi ya Roho Mutakatifu. Musizarau ujumbe unaotoka kwa Mungu. Lakini muchunguze kila jambo na kushika lile linalokuwa jema. Muepuke ubaya wa kila namna. Mungu wa amani mwenyewe awatakase kabisa, alinde uzima wenu wote ndiyo roho, moyo na mwili wenu, kusudi visikutiwe na kosa wakati Bwana wetu Yesu Kristo atakaporudia. Yule anayewaita ninyi atatimiza mambo hayo, kwa maana yeye ni mwaminifu. Wandugu, mutuombee vilevile. Musalimiane kwa upendo wa kikristo. Ninawasihi kwa jina la Bwana, musome barua hii kwa wandugu wote. Tunawatakia neema kutoka kwa Bwana wetu Yesu Kristo. Barua hii inatoka kwangu, mimi Paulo na kwa Silvano na Timoteo. Tunawaandikia ninyi kanisa la Tesalonika munaoungana na Mungu Baba yetu na Bwana Yesu Kristo. Tunawatakia neema na amani kutoka kwa Mungu Baba na kwa Bwana Yesu Kristo. Wandugu, tunapaswa kumushukuru Mungu siku zote kwa ajili yenu. Inatufaa kufanya vile kwa maana imani yenu inaongezeka, nao upendo wenu ninyi kwa ninyi unazidi kuongezeka. Kufuatana na ile, sisi tunajivuna kwa ajili yenu katika makanisa ya Mungu kwa sababu ya uvumilivu wenu na imani munayokuwa nayo katika mateso na taabu munazopata. Hayo yote yanahakikisha kwamba hukumu ya Mungu ni ya haki na matokeo yake ni kwamba ninyi munastahili kuingia katika Ufalme wake ambao kwa ajili yake ninyi munateseka. Kwa maana, Mungu yuko na haki ya kuwatesa wale wanaowatesa ninyi, na kuwapumzisha ninyi munaoteswa pamoja nasi. Jambo lile litatendeka wakati Bwana Yesu atakapoonekana tokea mbinguni pamoja na wamalaika wake wenye uwezo, katikati ya ndimi za moto kwa kuazibu wale wanaokataa kumujua Mungu na wale wasiokubali Habari Njema ya Bwana wetu Yesu. Azabu yao itakuwa kuangamizwa kwa milele, na kutengwa mbali na uso wa Bwana na mbali na utukufu wa uwezo wake, atakapokuja apate kutukuzwa na watu wake na kushangiliwa na wale wote wanaoamini. Ninyi vilevile mutakuwa pamoja nao kwa maana mumeamini habari tuliyowatangazia. Kwa sababu hii tunawaombea siku zote kusudi Mungu wetu awawezeshe kustahili kuishi kufuatana na mwito wake. Tunaomba kwamba kwa uwezo wake atimize nia zenu zote njema na kukamilisha kazi yenu ya imani. Kwa hivi mutatukuza jina la Bwana wetu Yesu, nanyi mutatukuzwa naye kwa neema ya Mungu wetu na ya Bwana Yesu Kristo. Sasa tunawaandikia juu ya mambo yanayoelekea kurudia kwa Bwana wetu Yesu Kristo na namna sisi tutakavyokusanyika mbele yake. Wandugu, tunawasihi sana, musifazaike upesi wala kuogopa kwamba Siku ya kurudi kwa Bwana imekwisha kutimia. Inawezekana munafahamu mambo yale kwa njia ya unabii, mahubiri na barua inayosemeka kwamba imetoka kwetu. Musikubali kudanganywa na mutu yeyote kwa namna yoyote. Kwa maana Siku ile haitatimia mpaka kwanza ule uasi mukubwa utokee na yule Mwovu aonekane ambaye mwisho wake ni kuangamizwa. Yeye atapinga kitu chochote watu wanachohesabu kuwa cha kimungu au wanachoabudu na kujiweka kuwa juu ya vyote. Yeye ataenda hata kuingia katika hekalu la Mungu na kukaa mule na kujiita mwenyewe kuwa Mungu. Hamukumbuki kwamba niliwaambia maneno haya wakati nilipokuwa pamoja nanyi? Lakini munajua kitu kinachozuiza mambo haya kutokea sasa. Kwa hivi yule Mwovu atatokea kwa wakati wake uliopangwa. Hata hivi yule Mwovu anatenda kazi zake kwa siri; lakini yule anayezuiza ataendelea hata atakapoondoshwa. Halafu, yule Mwovu atatokea, lakini Bwana Yesu atakapotokea atamwua kwa pumzi ya kinywa chake na kumwangamiza kwa nguvu za kumetameta kwake. Mwovu atakuja na uwezo wa Shetani na kufanya miujiza ya kila namna, vitambulisho na maajabu ya uongo. Atatumia ubaya wa kila namna kwa kuwadanganya wale wanaopotea kwa sababu hawakupenda kukubali na kupenda mambo ya kweli yaliyoweza kuwaokoa. Kwa sababu hii Mungu amewaweka chini ya nguvu ya upotovu wapate kuamini mambo ya uongo. Kwa hivi wale wote wasioamini maneno ya ukweli, waliofurahia mambo mabaya watahukumiwa. Lakini sisi tunapaswa kumushukuru Mungu siku zote kwa ajili yenu ninyi wandugu wapendwa wa Bwana. Kwa maana Mungu amewachagua ninyi wa kwanza kuwa watu wake kusudi mupate kuokolewa kwa kutakaswa na Roho Mutakatifu na kwa kuamini maneno ya ukweli. Mungu amewaalika kuwa vile kwa njia ya Habari Njema tuliyowatangazia, kusudi mupate kushiriki katika utukufu wa Bwana wetu Yesu Kristo. Basi wandugu, musimame imara na mushike mafundisho yetu tuliyowatolea, ikiwa kwa mahubiri au kwa barua yetu. Bwana wetu Yesu Kristo mwenyewe na Mungu Baba yetu, aliyetupenda na kwa neema yake akatufariji kwa milele na kutupatia tumaini njema, awafariji na kuwaimarisha katika matendo na maneno yote mema. Kwa mwisho wandugu, mutuombee, kusudi neno la Bwana lisambae upesi na kutukuzwa, kama vile inavyokuwa kwenu. Vilevile mumwombe Mungu kusudi atuopoe toka mikono ya watu wabaya na waovu. Kwa maana si watu wote wanaokubali kuamini Habari Njema. Lakini Bwana ni mwaminifu, atawaimarisha na kuwakinga na yule Mwovu. Bwana anatupatia tumaini kwa ajili yenu kwamba munafanya na mutaendelea kufanya yale tunayowaagiza. Bwana aongoze mafikiri yenu katika upendo wa Mungu na katika uvumilivu tunaopewa na Kristo. Wandugu, tunawaagiza katika jina la Bwana wetu Yesu Kristo kwamba mujitenge na wandugu wote wanaokuwa wavivu na wasiofuata mafundisho tuliyowapa. Munajua vizuri ninyi wenyewe namna munavyopaswa kuiga mufano wetu. Kwa maana sisi hatukukuwa wavivu wakati tulipoishi pamoja nanyi. Sisi hatukukula chakula cha mutu kwa bure, lakini tulitumika na kuchoka sana. Tulitumika muchana na usiku kusudi tusilemee hata mutu mumoja kati yenu. Tulifanya vile si kwa sababu hatukukuwa na haki ya kupokea musaada wenu, lakini kwa sababu tulitaka sisi wenyewe kuwa kwenu mufano wa kuiga. Kwa maana, wakati tulipokuwa kwenu, tulikuwa tunawaagiza hivi: “Mutu yeyote asiyetaka kutumika, na hapaswi kula vilevile.” Tunasema hivi kwa sababu tumepata habari kwamba wamoja kati yenu ni wavivu; hawatumiki, isipokuwa tu kujiingiza katika maneno ya wengine. Tunawaagiza watu wale na kuwaonya kwa jina la Bwana Yesu Kristo kwamba watumike katika utulivu kwa kujitoshelea wenyewe katika maisha yao. Lakini ninyi, wandugu, musichoke kutenda mema. Kama mutu hataki kushika maagizo tunayowatolea katika barua hii, mumwangalie vizuri mutu yule, musishirikiane naye, kusudi apate haya. Musimuhesabu kama vile adui, lakini mumwonye kama vile ndugu. Bwana wa amani mwenyewe awape amani siku zote na kwa njia zote. Bwana akuwe pamoja nanyi wote. Hii ni salamu ninayoiandika kwa mukono wangu mimi Paulo mwenyewe. Hii ndiyo sahihi yangu katika kila barua yangu, na mwandiko wangu. Tunawatakia ninyi wote neema kutoka kwa Yesu Kristo. Barua hii inatoka kwangu mimi Paulo, niliyeitwa kuwa mutume wa Kristo Yesu kwa amri ya Mungu Mwokozi wetu na ya Kristo Yesu tunayemutumainia. Ninakuandikia wewe Timoteo mwana wangu wa kweli katika imani. Ninakutakia neema na rehema na amani kutoka kwa Mungu Baba yetu na kwa Kristo Yesu Bwana wetu. Ukae kule Efeso sawa vile nilivyokusihi wakati nilipokwenda Makedonia. Na kule uwazuize wale watu wanaofundisha mafundisho ya uongo. Uwaambie wasishikamane na hadisi za uongo, pamoja na mambo yasiyokuwa na mwisho ya wababu. Hayo yote yanaleta mabishano, wala hayafai kitu kwa kutimiza mupango wa Mungu wa wokovu, unaojulikana kwa njia ya imani. Shabaha ya agizo hilo ni kusudi kuwe upendo unaotokana na moyo safi na zamiri nzuri na imani ya kweli. Watu wamoja wamekosa kuwa na tabia hiyo hata wamefuata maneno ya ovyo ovyo. Wanataka kuwa walimu wa Sheria ya Musa, lakini hawaelewi wao wenyewe maneno wanayosema wala maneno wanayohakikisha. Tunajua kwamba Sheria ni nzuri, kama ikitumiwa kwa njia ya haki. Vilevile ni sherti kujua kwamba Sheria haikuwekwa kwa ajili ya wenye haki, lakini kwa ajili ya watenda mabaya, waasi, watu wasiomuheshimu Mungu, wenye zambi, nao wenye kuchafua vitu vitakatifu na kukufuru, na kwa ajili ya wale wanaowaua wababa zao au wamama zao, na wauaji wowote. Sheria imewekwa kwa ajili ya waasherati, wanaume wanaozini wao kwa wao, wenye kuuzisha watu, wasema uongo, wale wanaofanya viapo vya uongo na kwa ajili ya wote wanaofanya matendo yanayokuwa umbalimbali na mafundisho ya kweli. Mafundisho haya yanalingana na Habari Njema ya utukufu wa Mungu mwenye baraka, ambayo nilipewa nipate kuihuburi. Ninamushukuru Bwana wetu Kristo Yesu aliyenitia nguvu, kwa sababu alinihesabu kuwa mwaminifu hata akaniweka kwa kazi yake. Ingawa zamani nilikuwa mwenye kumutukana, mwenye kumutesa na kumutendea kwa ukali, lakini amenihurumia, kwa sababu yote niliyofanya, niliyafanya kwa upumbafu kwa maana sikukuwa bado na imani. Bwana wetu amenijalia neema kwa uwingi, amenipa imani na upendo tunaokuwa nao katika kuungana kwetu na Kristo Yesu. Neno hili ni la kuaminiwa nalo linastahili kukubaliwa kabisa: Kristo Yesu alikuja katika dunia kwa kuokoa wenye zambi. Na mimi ni wa kwanza mwenye zambi kati yao, lakini kwa sababu hiyo Mungu amenihurumia. Alifanya vile kusudi kwa njia yangu mimi ninayekuwa mutenda zambi wa kwanza, Yesu Kristo apate kuonyesha uvumilivu wake. Na hivi mimi nipate kuwa mufano kwa wote watakaoamini nyuma na kupata uzima wa milele. Kwa Mufalme wa milele, asiyeweza kufa, asiyeonekana, Mungu peke yake, ikuwe heshima na utukufu milele na milele! Amina. Timoteo mwana wangu, ninakupa agizo hili kufuatana na maneno ya unabii yaliyosemwa zamani juu yako. Maneno hayo ndiyo yatakayokuwezesha kupiga vita nzuri, ukichunga imani yako na kuwa na zamiri safi. Watu wamoja wamekataa kuwa na zamiri hata wamepoteza imani yao. Kati yao kuna Himeneo na Alesanduro, ambao nimemwachia Shetani kusudi wasimutukane Mungu tena. Mbele ya yote, ninawaonya ninyi kuwaombea watu wote. Muombe Mungu awasaidie na kuwabariki, na mumushukuru kwa ajili yao. Inafaa kuombea wafalme na watu wenye mamlaka kusudi tupate kuishi katika ukimya na amani katika kushikamana na ibada na katika mwenendo safi. Nalo jambo hilo ni zuri na lenye kupendeza Mungu Mwokozi wetu, anayetaka watu wote waokolewe na kuweza kutambua ukweli. Kwa maana kuna Mungu mumoja tu, na kuna mupatanishi mumoja tu kati ya Mungu na watu, ni yule mutu, Kristo Yesu, aliyejitoa mwenyewe kusudi awakomboe watu wote. Na huo ni ushuhuda kwa wakati uliopangwa, kwamba Mungu anataka kuwaokoa watu wake. Ni kwa hiyo nimewekwa kuwa mujumbe na mutume kwa kuwafundisha watu wa mataifa mengine kusudi wapate kumwamini Mungu na kutambua ukweli. Mimi ninasema ukweli wala si uongo. Basi, ninataka watu waombe Mungu wakiinua mikono juu, ikiwa imetakaswa, nao wafanye vile bila kasirani wala ubishi. Ninataka vilevile wanawake wavae kwa namna inayostahili. Inafaa wajipambe kwa adabu na kwa ukadirifu, si kwa namna mbalimbali za urembo za kusuka nywele, wala kwa zahabu, wala kwa ushanga au nguo za bei kali. Lakini kujipamba kwao kuwe matendo mema yanayostahili kutendwa na wanawake wanaojidai kwamba wanajitoa kwa kumwabudu Mungu. Wanawake wanapaswa kusikiliza mafundisho katika ukimya na utii kabisa. Lakini simupatii mwanamuke ruhusa ya kufundisha, wala ya kumutawala mwanaume, lakini akae katika ukimya. Kwa maana, Adamu ndiye aliyeumbwa wa kwanza, na kisha Eva. Na si Adamu aliyedanganywa, lakini ni mwanamuke ndiye aliyedanganywa na kuasi agizo la Mungu. Ingawa hivi mwanamuke ataokolewa kwa kuzaa watoto, kama akidumu katika imani, upendo na utakatifu na kuwa mukadirifu. Neno hili ni la kweli; kama mutu anatamani kazi ya musimamizi wa kanisa anatamani kazi nzuri. Basi musimamizi wa kanisa anapaswa kuwa mutu asiyeshitakiwa neno lolote. Sherti akuwe na muke mumoja tu, akuwe mukadirifu, mwenye akili, akuwe mwema na mwenye kupenda kukaribisha wageni na mwenye kujua kufundisha. Hapaswi kuwa mulevi wala mupiganaji, lakini akuwe mupole mwenye kupenda amani, wala asikuwe mutu wa kupenda feza. Anapaswa kuwa mutu mwenye kuongoza jamaa yake vizuri na kuadibisha watoto wake kusudi wakuwe wenye utii na wenye heshima kabisa. Kwa maana mutu anayeshindwa na kuongoza jamaa yake mwenyewe, namna gani ataweza kuchunga kanisa la Mungu? Yeye hapaswi kuwa mwamini mupya; kusudi asitawaliwe na kiburi na kuhukumiwa kama vile Shetani alivyokuwa. Vilevile inafaa akuwe mutu mwenye kushuhudiwa vizuri na watu wa inje ya kanisa, kusudi asizarauliwe na kunaswa katika mutego wa Shetani. Vilevile wasaidizi wanaotumika katika kanisa wanapaswa kuwa watu wenye heshima. Hawapaswi kuwa wenye nia mbili katika masemi yao wala wenye kunywa pombe kwa uwingi wala wenye kutafuta mali kwa njia isiyokuwa sawa; wanapaswa kushikamana kwa zamiri safi na ukweli wa imani uliofunuliwa. Inafaa wapimwe kwanza, na kisha kama hawakuonekana na kosa, wataweza kutumika kama wasaidizi wa kanisa. Wanawake wao wanapaswa kuwa na adabu vilevile, wasikuwe wasingiziaji wa uongo, lakini wakuwe wakadirifu na waaminifu katika mambo yote. Inafaa wasaidizi wa kanisa wakuwe kila mutu na muke mumoja tu, na wanapaswa kuwa watu wenye kuongoza vizuri watoto wao pamoja na jamaa zao. Wasaidizi wanaotumika vizuri kazi zao, wanajiheshimisha, na wanaweza kutangaza kwa uhodari habari za imani tunayokuwa nayo katika kuungana na Kristo Yesu. Ninakuandikia barua hii, ijapokuwa ninatumaini kuja kukuona kisha muda kidogo. Lakini, kama nikikawia kufika, utaweza hivi kujua mwenendo unaopaswa kuwa nao katika nyumba ya Mungu, maana yake katika jamaa ya Mungu Mwenye Uzima. Yeye ndiye anayekuwa nguzo na musingi wa kweli. Hakika siri ya ibada yetu ni kubwa: Yeye alitokea kwa mufano wa mutu, alishuhudiwa na Roho Mutakatifu kuwa mwenye haki. Alionekana na wamalaika. Alitangazwa katikati ya mataifa. Aliaminiwa popote katika dunia. Na alinyanyuliwa mbinguni katika utukufu. Roho Mutakatifu anasema wazi kwamba katika nyakati za mwisho, watu wengine watapotoka katika imani yao na kufuata roho za udanganyifu na mafundisho ya pepo. Wanadanganywa na watu wenye uongo na wanafiki wenye zamiri iliyokufa, iliyoharibika kabisa kama vile imeteketezwa kwa moto. Wao wanafundisha kwamba ni vibaya kuoana, na wanawakataza watu kula vyakula fulani fulani. Lakini Mungu aliumba vyakula vile kusudi watu waliokwisha kumwamini na kutambua ukweli wapate kuvitumia wakisha kumushukuru. Kila kitu Mungu alichokiumba ni kizuri, wala hakuna kile kinachopaswa kukataliwa, lakini inafaa kumushukuru Mungu mbele ya kukikula. Kwa maana kwa njia ya neno la Mungu na ya maombi, chakula kinatakaswa mbele yake. Kama ukiwaelezea waziwazi wandugu maneno hayo, utakuwa mutumishi mwema wa Kristo Yesu, mwenye kukulishwa kiroho na maneno ya imani na mafundisho mazuri uliyoshika kabisa. Lakini ukatae hadisi za uongo zilizotungwa na wanawake wazee. Ujizoeze katika maisha yako kumwabudu Mungu kwa ukweli. Mazoezi ya mwili yana mafaa kidogo, lakini kushikamana na ibada kuna mafaa katika mambo yote, kwa maana kunatupatia ahadi ya kuishi kwa wakati huu wa sasa na kwa wakati utakaokuja. Neno hilo ni la kuaminiwa, nalo linastahili kukubaliwa kabisa. Na ni kwa hiyo tunasumbuka na kupigana, kwa maana tunamutumainia Mungu Mwenye Uzima, Mwokozi wa watu wote na hasa zaidi Mwokozi wa waamini. Hayo ndiyo maneno unayopaswa kuagiza na kufundisha. Usijiachilie kuzarauliwa na mutu yeyote kwa sababu ungali bado kijana. Lakini ukuwe mufano kwa waamini, katika masemi yako, katika mwenendo wako, katika upendo, katika imani na katika maisha safi. Kwa kungojea mpaka nitakapofika, ujitolee kwa kuwasomea watu Maandiko Matakatifu kwa kuwaonya na kuwafundisha. Usiache kutumia ile zawadi ya kiroho inayokuwa ndani yako, uliyopokea kutokana na maneno ya manabii na kwa njia ya kuwekewa mikono na wazee wa kanisa. Ufikiri sana juu ya mambo hayo na ujitolee kwa kuyatimiza hata watu wote waone waziwazi maendeleo yako. Ujiangalie wewe mwenyewe na kuangalia mafundisho yako, nawe ushikamane nayo. Kwa maana ukifanya hivi, utajiokoa wewe mwenyewe na kuokoa wale wanaokusikiliza. Usimukaripie muzee kwa nguvu, lakini umwonye kama baba yako. Uwatendee vijana wanaume kama wandugu zako, nao wanawake wazee kama mama yako na vijana wanawake kama wadada zako, ukijilinda katika maisha safi. Uwaheshimu wanawake wajane wasiokuwa na tegemeo lolote. Lakini kama mujane akiwa na watoto au wajukuu, inafaa wajifunze kwanza kutimiza mapaswa yao ya kidini kwa ajili ya jamaa zao wenyewe na kuwarudishia wazazi na babu zao mema waliyowatendea, kwa maana jambo hilo linamupendeza Mungu. Mujane wa kweli asiyekuwa na mutu yeyote wa kumusaidia, anamutumainia Mungu, na kudumu kumutolea mahitaji yake na kumwomba muchana na usiku. Lakini mujane anayeishi katika tamaa mbaya amekwisha kufa, ijapokuwa angali bado muzima. Hayo ndiyo maneno unayopaswa kuwaagiza wajane kusudi wasikuwe na mashitaki. Kama mutu asipotunza wandugu zake na hasa zaidi watu wa jamaa yake mwenyewe, huyu amekana imani yake naye ni mubaya kuliko mupagani. Usimwandike katika hesabu ya wajane mujane yeyote ambaye hajatimiza umri wa miaka makumi sita. Tena inafaa akuwe yule aliyeolewa na mume mumoja tu. Sherti ajulikane kwa matendo yake mema. Anapaswa kuwa mutu aliyeadibisha watoto wake vizuri, aliyekaribisha wageni, aliyewapokea watu wa Mungu akiwanawisha miguu, aliyewasaidia wenye taabu na aliyejitolea kwa kutenda mema ya kila namna. Lakini ukatae kuandika wajane wanaokuwa wangali vijana katika hesabu ile kwa maana wanapovutwa na tamaa ya kutaka kuolewa, wanaacha kumutumikia Kristo. Na kwa hiyo wanavunja agano walilofanya naye kwanza na kuanguka katika kosa. Na zaidi ya hiyo, wanashikwa na uvivu na kuwa na tabia ya kutangatanga nyumba kwa nyumba. Na si ile tu, vilevile wao ni wakatetea na wenye kujiingiza katika maneno ya watu wengine na kusema maneno yasiyofaa. Kwa sababu hiyo, ninataka wajane wanaokuwa wangali vijana waolewe, wazae watoto na kutunza nyumba zao, kusudi waadui wasipate nafasi ya kutuchongea. Kwa maana wajane wamoja wamekwisha kupotoka na kumufuata Shetani. Lakini kama mwamini yeyote akiwa na wajane katika jamaa lake, anapaswa kuwasaidia kusudi kanisa lisilemewe. Na hivi kanisa nalo litaweza kuwasaidia wale wajane wasiokuwa na tegemeo lolote. Wazee wa kanisa wanaoongoza kazi yao vizuri wanastahili kupokea mushahara mara mbili, hasa zaidi wale wanaojitolea kwa kufanya kazi ya kuhubiri na kufundisha. Kwa maana Maandiko Matakatifu yanasema: “Usifunge kinywa cha ngombe anapokanyaga ngano.” Na tena yanasema: “Mutumishi anastahili kupewa mushahara wake.” Ukatae mashitaki juu ya muzee isipokuwa kwa ushuhuda wa watu wawili au watatu. Wale wenye kufanya zambi, uwakaripie mbele ya watu kusudi wengine wapate kuogopa vilevile. Ninakuagiza mbele ya Mungu na mbele ya Kristo Yesu na ya wamalaika watakatifu, ushike kanuni hizo bila kuwazia mutu kitu wala kuwa na upendeleo katika mambo yote unayofanya. Usiweke mikono juu ya mutu kwa haraka, wala usishiriki zambi za watu wengine. Ujilinde wewe mwenyewe katika maisha safi. Kwa ajili ya maumivu ya tumbo lako na uzaifu wa mwili wako wa kila mara, tangu sasa usikunywe maji tu, lakini utumie divai kidogo. Zambi za watu wamoja zinaonekana waziwazi hata mbele hawajahukumiwa. Lakini zambi za wengine zinajulikana kisha. Na ni hivi vilevile, matendo mazuri yanaonekana waziwazi, na hata yale yasiyoonekana wazi hayawezi kufichwa. Watu wote wanaokuwa watumwa wanapaswa kuwaheshimu wabwana wao kabisa, kusudi watu wasitukane jina la Mungu na kuzarau mafundisho yetu. Na wale wanaokuwa na wabwana waamini, wasiwakosee heshima kwa sababu wao ni wandugu. Wanapaswa kuwatumikia vizuri zaidi, kwa maana wao ni wandugu waamini na wapendwa, nao wanashiriki faida ya kazi yao. Hayo ndiyo maneno unayopaswa kufundisha na kuhubiri. Kama mutu akifundisha mafundisho mengine, naye hakubali maneno ya kweli ya Bwana wetu Yesu Kristo wala mafundisho yanayolingana na dini yetu, yeye anajaa majivuno wala hajui kitu. Yeye yuko na ulema wa kubishana na kugombezana juu ya maana ya maneno. Na hayo yanaleta wivu, makelele, matukano, masingiziano na magomvi yasiyokuwa na mwisho ya watu wenye akili iliyokwisha kupotoka hata wamesahau ukweli kabisa. Ndio wale wanaozani kwamba dini ni njia ya kupata utajiri. Hakika, dini ni pato kubwa kwa mutu kama anafurahia vitu anavyokuwa navyo. Kwa maana hatukuleta kitu katika dunia wala hatuwezi kurudia na kitu. Basi kama tukiwa na chakula na nguo, vile vinatosha. Lakini wale wanaotaka kuwa watajiri wanaanguka katika majaribu na mitego, na katika tamaa nyingi za upumbafu na mabaya zinazowatumbukiza katika anguko na uharibifu. Kwa maana kupenda feza ni shina la mabaya yote. Kwa ajili ya kuzitamani watu wamoja wanaanguka katika imani yao, na wanajiumiza mioyo wakijiletea huzuni nyingi. Lakini wewe mutu wa Mungu, uepuke mambo haya, ushikamane na haki, ibada, imani, upendo, uvumilivu na upole. Upigane vita nzuri kwa kuchunga imani yako, upate kujitwalia uzima wa milele Mungu aliokuitia wakati ulipoitikia imani yako mbele ya washuhuda wengi. Mbele ya Mungu anayevipatia vitu vyote uzima, na mbele ya Kristo Yesu aliyetoa ushuhuda wa kweli mbele ya Pontio Pilato, ninakuagiza maneno haya: ushike mambo uliyoagizwa kwa uaminifu bila kosa mpaka Siku Bwana wetu Yesu Kristo atakapotokea. Kutokea kwake kutafanywa na Mungu kwa wakati aliopanga. Yule ndiye Mungu anayestahili kutukuzwa, anayekuwa peke yake mutawala, mufalme wa wafalme na Bwana wa wabwana. Ni yeye tu asiyeweza kufa na anayekaa katika mwangaza ambao mutu hawezi kukaribia. Hakuna mutu aliyemwona wala hakuna mutu anayeweza kumwona. Ndiye mwenye heshima na uwezo wa milele! Amina. Uwaagize wale wanaokuwa watajiri katika dunia hii ya sasa wasijivune, vilevile wasiweke matumaini yao katika mali inayotoweka upesi. Lakini wamutumainie Mungu anayetupatia vitu vyote kwa uwingi kusudi tufurahiwe navyo. Uwaagize watende mema, wakuwe watajiri katika matendo mazuri, nao wasaidiane kwa moyo safi na kushiriki mali yao na wengine. Kwa njia hii, watajiwekea akiba nzuri na yenye kudumu kwa ajili ya siku zitakazokuja kusudi wapate uzima wa kweli. Timoteo, uchunge vizuri kile ulichopewa kwa kulinda, ukiepuka maneno ya kidunia na mabishano yasiyokuwa na maana juu ya ile watu wengine wanayoita kuwa ni elimu lakini ni uongo. Kwa ajili ya kufuata elimu ile, watu wamoja wamepotoka katika imani yao. Ninawatakia neema kutoka kwa Mungu. Barua hii inatoka kwangu mimi Paulo, niliyeitwa kuwa mutume wa Kristo Yesu kwa mapenzi ya Mungu, kwa kutangaza ahadi ya uzima tunaokuwa nao katika kuungana na Yesu Kristo. Ninakuandikia wewe Timoteo, mwana wangu mupendwa. Ninakutakia neema, rehema, na amani kutoka kwa Mungu Baba na kwa Bwana wetu Kristo Yesu. Ninamushukuru Mungu ambaye ninamutumikia kwa zamiri safi kama vile babu zangu walivyofanya, ninapokukumbuka siku zote katika maombi yangu usiku na muchana. Nikikumbuka machozi yako, ninatamani sana kukuona kusudi nipate kujazwa na furaha. Ninakumbuka vilevile imani yako isiyokuwa ya udanganyifu, imani ile tate muzaa mama yako Loisi na mama yako Euniki waliyokuwa nayo. Ninajua hakika kwamba wewe vilevile uko nayo. Kwa sababu hii ninakukumbusha uchochee zawadi ya Mungu uliyoipokea nilipoweka mikono juu yako. Kwa maana Mungu hakutupatia sisi Roho wa kuogopa, lakini Roho anayetupatia nguvu, upendo na kujizuiza. Basi, usisikie haya ya kutoa ushuhuda kwa ajili ya Bwana wetu, wala usisikie haya kwa sababu yangu mimi ninayekuwa katika kifungo kwa ajili yake. Lakini ushiriki nami katika mateso kwa ajili ya Habari Njema, kufuatana na uwezo unaopewa na Mungu. Yeye ndiye aliyetuokoa na kutuita kuwa watu wake, si kwa sababu ya matendo lakini ni kwa sababu ya mupango wake mwenyewe na neema yake aliyotupatia katika kuungana na Kristo Yesu mbele ya nyakati zote. Lakini neema hii imeonekana sasa kwa kuja kwa Mwokozi wetu Kristo Yesu. Yeye ameshinda nguvu za lufu na kwa njia ya Habari Njema ameonyesha wazi uzima wa milele. Kwa ajili ya Habari Njema hii, nimewekwa kuwa mujumbe, mutume na mwalimu, na kwa sababu hiyo ninapata mateso haya. Lakini sisikii haya kwa ajili ya ile. Maana ninajua ni nani yule niliyemwamini, nami ninahakikisha kwamba anaweza kuchunga kile alichonipa kwa kunilinda mpaka Siku ile ya kurudi kwake. Ushike maneno ya kweli niliyokufundisha, yapate kuwa mufano kwako. Ushikamane na imani na upendo unaokuwa nao kwa njia ya kuungana kwako na Kristo Yesu. Kwa nguvu za Roho Mutakatifu anayekaa ndani yetu, uchunge kile kitu kizuri ulichopewa kwa kulinda. Kama unavyojua wewe mwenyewe, watu wote wa jimbo la Azia wameniacha; kati yao kuna Figelo na Hermogene. Bwana awajalie mema sana watu wa jamaa ya Onesiforo, kwa maana amekuja mara nyingi kunifariji, wala hakusikia haya kwa kuniona niko katika kifungo. Wakati alipofika Roma, alinitafuta kwa bidii sana mpaka akaniona. Bwana amusikilie huruma kwa Siku ile! Unajua vizuri sana vilevile mambo yote aliyonitendea kule Efeso. Basi wewe mwana wangu, ukuwe hodari kwa njia ya neema uliyopata katika kuungana kwako na Kristo Yesu. Wewe umesikia mafundisho niliyotoa mbele ya washuhuda wengi. Nawe sasa uyafundishe kwa watu waaminifu watakaoweza vilevile kuyatoa kwa watu wengine. Ushiriki katika mateso kama vile askari mwema wa Kristo Yesu. Askari anapokuwa katika vita, hapaswi kushugulika na mambo ya kawaida ya maisha ya wakaaji kama anataka kumupendeza mukubwa wa kundi lake. Vilevile mutu yeyote anayeshindana katika michezo hawezi kupata zawadi ya ushindi kama asipotii kanuni za michezo. Tena mulimaji anayetumika kazi ngumu ndiye anayepaswa kupata sehemu ya kwanza ya mavuno. Ufikiri juu ya maneno hayo ninayosema, kwa maana Bwana atakupa uwezo kwa kuyaelewa yote. Umukumbuke Yesu Kristo aliyekuwa wa ukoo wa mufalme Daudi, na aliyefufuka sawa vile inavyotangazwa na Habari Njema hii ninayohubiri. Mimi ninateswa na kufungwa sawa mutenda maovu kwa sababu ninahubiri Habari Njema hii. Lakini Neno la Mungu halifungwi. Ni kwa hiyo ninavumilia mambo yote kwa ajili ya watu ambao Mungu alijichagulia kuwa wake, kusudi wao vilevile wapate kuokoka na kupata utukufu wa milele unaopatikana kwa njia ya Kristo Yesu. Maneno haya ni ya kuaminiwa: Kama tumekufa pamoja naye, tutaishi pamoja naye vilevile. Kama tunaendelea kuvumilia, tutatawala pamoja naye vilevile. Kama tunamukana, naye atatukana vilevile. Kama tunakosa kuwa waaminifu, yeye anabaki mwaminifu. Kwa maana hawezi kujikana yeye mwenyewe. Uwakumbushe watu maneno hayo yote na kuwaonya wazi mbele ya Mungu waache kubishana juu ya maneno. Mabishano hayana faida kwa maana yanawapoteza wale wanaoyasikia. Ufanye juhudi kusudi upate kuhesabiwa mbele ya Mungu kama mutu anayemupendeza, ukiwa kama mutumishi asiyesikia haya juu ya kazi yake, lakini anayetangaza kwa haki ujumbe wa kweli wa Mungu. Uepuke masemi yasiyokuwa na maana na ya kidunia, kwa maana wale wanaoyafuata wanazidi kupotoka katika ibada ya uongo. Maneno yao yanaambukiza kama vile kidonda chenye kuoza kinavyoharibu mwili wote. Kati yao kuna Himeneo na Fileto. Hao wamepotoka mbali na ukweli, wamepotosha imani ya watu wengi wakisema kwamba ufufuko tunaongojea umekwisha kufanyika. Lakini musingi uliojengwa na Mungu, unasimama imara. Nayo maneno haya yamechapwa juu ya musingi ule “Bwana anajua wale wanaokuwa wake,” na haya mengine: “Kila mutu anayesema kwamba yeye ni wa Bwana anapaswa kujitenga na maovu.” Ndani ya nyumba kubwa, hamuna vyombo vya zahabu na feza tu, lakini muko vilevile vyombo vya miti na vya udongo. Vimoja ni vya matumizi ya kipekee na vingine ni vya matumizi ya kawaida. Basi kama mutu atajitakasa kwa kujitenga na maovu hayo yote atakuwa chombo cha matumizi ya kipekee, kitakatifu cha mwenye nyumba na chenye mafaa kwake na kuwa tayari kwa kila kazi njema. Ujiepushe na tamaa za ujana, utafute kuishi katika haki, imani, upendo na amani pamoja na watu wote wanaomwabudu Bwana kwa moyo safi. Ukatae mabishano ya kipumbafu na yasiyokuwa na maana; unajua wewe mwenyewe kwamba yanaleta magomvi. Basi, mutumishi wa Bwana hapaswi kugombana. Anapaswa kuwa mupole kwa watu wote, anayejua kufundisha na muvumilivu. Anapaswa kuwaonya kwa upole wale wanaopingana naye; kwa maana labda Mungu anaweza kuwajalia hata wapate kugeuka toka zambi na kutambua ukweli. Kwa njia hiyo wanaweza tena kupata ufahamu na kuponyoka katika mitego ya Shetani, aliyewanasa na kuwafanya watimize mapenzi yake. Ujue vizuri kwamba siku za mwisho zitakuwa nyakati za magumu. Kwa maana watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda feza, wenye kujisifu na wenye kiburi, wenye kukufuru, wasiotii wazazi wao, wasioshukuru na waovu. Hawatakuwa na upendo wala huruma. Watakuwa wenye kusingiziana, wasiojizuiza, wakali na wasiopenda mema. Watakuwa wenye kutoana, wenye kichwa kigumu, wenye majivuno na wenye kupenda tamaa ya vitu kuliko kumupenda Mungu. Kwa inje watajionyesha kama watu wenye kushikamana na ibada, lakini wanazarau uwezo wake. Ujiepushe na watu hao. Kwa maana kati yao kuna wamoja wanaojiingiza katika nyumba za watu na kuwashawishi wanawake wajinga wanaolemewa na mizigo ya zambi na kuvutwa na tamaa za namna nyingi. Wanawake wale wanataka kujifunza siku zote, lakini hawafikii kutambua ukweli. Watu wale wanapinga ukweli kama vile Yane na Yambure walivyopingana na Musa. Akili ya watu hao imepotoka, nayo imani yao imegeuka bure. Lakini hawataendelea mbali sana, kwa sababu upumbafu wao utaonekana wazi mbele ya watu wote, sawa ilivyokuwa kwa Yane na Yambure. Lakini wewe umefuata kabisa mufano wangu katika mafundisho yangu na mwenendo wangu, makusudi yangu, imani yangu, uvumilivu wangu, upendo wangu, ungojevu wangu, mateso na taabu yangu. Unajua mambo yote ambayo yalinitokea kule Antiokia, Ikonio na Listra. Mateso haya niliyavumilia, na Bwana akaniokoa katika yote. Nao wote wanaotaka kuishi maisha ya kumwabudu Mungu katika kuungana na Kristo Yesu, watateswa. Lakini watu waovu na wadanganyifu wataendelea katika maovu, wakipotosha watu wengine na kujipotosha wenyewe. Lakini wewe ushikamane na mambo yale uliyofundishwa na kuyaamini kabisa. Unajua ni nani aliyekufundisha. Tena, tangia utoto wako unajua Maandiko Matakatifu yanayoweza kukupatia hekima kusudi uokolewe kwa njia ya kumwamini Kristo Yesu. Maandiko yote Matakatifu yameandikwa kwa maongozi ya Mungu na yanafaa kwa kufundisha, kuonya, kuhakikisha na kuadibisha katika haki, kusudi mutu wa Mungu apate kukamilika na kuwa tayari kabisa kwa kutenda kila kazi njema. Ninakuamuru mbele ya Mungu na mbele ya Kristo Yesu atakayewahukumu wazima na wafu na kufuatana na kurudi kwake kwa kutawala: utangaze Neno la Mungu kwa nguvu kwa wakati unaofaa na kwa wakati usiofaa. Ukaripe, usahihishe na kuonya ukifundisha kwa uvumilivu. Maana kutakuja wakati watu watakapokataa kusikiliza mafundisho ya kweli, lakini watafuata tamaa zao wenyewe wakijitafutia walimu wengi kwa kuwafundisha mambo yale wanayotamani kusikia. Watafunga masikio yao wasisikilize mambo ya kweli na kusikiliza hadisi za uongo. Lakini wewe, ujiangalie katika mambo yote, uvumilie mateso, ufanye kazi yako ya kuhubiri Habari Njema na kutimiza kabisa utumishi wako. Kwa maana, mimi sasa niko tayari kutolewa kama sadaka, na wakati wa kufa kwangu umekaribia. Nimeshindana vizuri, nimekimbia na kufika mwisho wa mashindano yangu. Nimelinda imani yangu. Tangia sasa nimetayarishiwa zawadi ya ushindi, ndiyo ile taji ya haki, ambayo Bwana anayekuwa Mwamuzi wa haki atakayonipa siku ile ya kurudi kwake. Wala hatanipa mimi peke yangu tu, lakini na wale wote wanaopenda kumwona wakati atakaporudi. Ufanye nguvu kufika kwangu upesi. Dema amependelea mambo ya dunia hii akaniacha na kwenda Tesalonika. Kreske akaenda Galatia, na Tito akaenda Dalmatia. Luka peke yake ndiye anayekuwa hapa pamoja nami. Umutwae Marko, ukuje pamoja naye, kwa sababu ananifalia katika kazi yangu. Nimemutuma Tikiko kule Efeso. Wakati utakapokuja uniletee koti niliyoacha kule Troa kwa Karpo; uniletee vilevile vitabu, hasa vile vya ngozi. Alesanduro, yule mufua vyuma amenitendea mabaya mengi. Bwana atamulipa kufuatana na matendo yake. Nawe vilevile ujilinde naye kwa sababu alipinga kwa nguvu maneno yetu yote. Nilipojitetea kwa mara ya kwanza hakuna hata mutu mumoja aliyenisaidia; wote waliniachilia. Mungu asiwahesabie makosa yao! Lakini Bwana alinisaidia, akanitia nguvu nipate kuitangaza Habari Njema kwa ukamilifu kusudi watu wa mataifa mengine wapate kuisikia. Nami nikaokolewa toka katika kinywa cha simba. Bwana ataniokoa toka katika mambo yote mabaya na kunipeleka salama katika Ufalme wake wa mbinguni. Bwana atukuzwe milele na milele. Amina. Unisalimie Prisila na Akila na jamaa la Onesiforo vilevile. Erasto alibakia Korinto, na nilimwacha Trofimo kule Mileto kwa sababu alikuwa mugonjwa. Ufanye nguvu kufika mbele ya wakati wa baridi kali. Eubulo, Pude, Lino, Klaudia na wandugu wote waamini wanakusalimia. Bwana akulinde. Ninawatakia neema kutoka kwa Mungu. Barua hii inatoka kwangu mimi Paulo, mutumishi wa Mungu na mutume wa Yesu Kristo. Mimi nimetumwa kwa kuongoza watu waliochaguliwa na Mungu wapate kumwamini na kutambua ukweli unaolingana na dini yetu. Na kwa njia hiyo watapata tumaini la uzima wa milele, ambalo Mungu asiyesema uongo alituahidi mbele ya mwanzo wa nyakati. Alifunua neno lake kwa wakati alioupanga kwa njia ya mahubiri ambayo yeye Mungu Mwokozi wetu aliyoniamuru kutangaza. Ninakutumia barua hii, wewe Tito, mwana wangu wa kweli katika imani tunayoshiriki pamoja. Ninakutakia neema na amani kutoka kwa Mungu Baba na kwa Yesu Kristo Mwokozi wetu. Nimekuacha katika kisanga cha Krete kusudi upate kutengeneza maneno yaliyobaki na kusimika wazee katika kanisa ndani ya kila muji, ukifuata maagizo niliyokutolea: muzee wa kanisa anapaswa kuwa mutu asiyeshitakiwa neno lolote. Sherti akuwe na muke mumoja nao watoto wake wanapaswa kuwa waamini na wasioshitakiwa neno juu ya mwenendo mubaya au juu ya kukosa utii. Kwa maana musimamizi wa kanisa anapaswa kuwa mutu asiyeshitakiwa neno, kwa sababu yeye ni mwangalizi wa kazi ya Mungu. Hapaswi kuwa mutu mwenye kiburi, wala mukali, mulevi, mugomvi wala mwenye kutafuta mali kwa njia mbaya. Lakini inafaa akuwe mwenye kupenda kukaribisha wageni, mwenye kupenda mema, mukadirifu, mwenye haki, mutakatifu na mutaratibu. Anapaswa kushika Neno la kweli linalolingana na mafundisho yetu. Hivi ataweza kuwaonya watu kwa njia ya mafundisho ya kweli na kuwashinda wale wanaomupinga. Kufuatana na hiyo, kuna watu wengi hasa kati ya Wayuda walioamini, wanaokuwa waasi, wakatetea na wadanganyifu. Inafaa kuwanyamazisha watu hao kwa sababu wanapotosha jamaa nzima kwa kufundisha mambo yasiyofaa wakitafuta kupata mali kwa njia mbaya. Na hata mumoja wa manabii wao wenyewe, Mukrete, alisema: “Wakrete ni wasema uongo siku zote, nyama wabaya, wavivu na walafi.” Ushuhuda huo ni wa kweli. Basi kwa hiyo uwaonye vikali, kusudi wapate kuwa na imani kamili. Na zaidi ya ile hawatafuata hadisi za uongo za Kiyuda wala maagizo ya watu waliopotoka mbali na ukweli. Kila kitu ni safi kwa watu wanaokuwa safi. Lakini hakuna chochote kinachokuwa safi kwa watu wachafu na wasiomwamini Mungu, kwa maana akili na zamiri zao zimekuwa chafu. Wanajidai kwamba wanamujua Mungu, lakini wanamukana kwa matendo yao. Wao ni wenye machukizo, waasi hata hawafai kwa kufanya kazi yo yote nzuri. Lakini kwa ngambo yako, ufundishe maneno yale yanayolingana na mafundisho ya kweli. Uwaambie wazee wanaume wakuwe wakadirifu, wenye heshima na utaratibu, wenye kukamilika katika imani, katika upendo na uvumilivu. Vilevile uwaambie wanawake wazee wakuwe na mwenendo unaostahili kwa watu watakatifu. Hawapaswi kuwa wasingiziaji, wala wasikuwe watumwa wa pombe, lakini wakuwe wenye kutoa mafundisho mazuri. Kwa njia hii wataweza kuwafundisha vijana wanawake kuwapenda waume wao na watoto wao, na kuwa wenye utaratibu, wenye maisha safi, wenye kutunza nyumba zao vizuri, wema na wenye kutii waume wao, kusudi Neno la Mungu lisitukaniwe. Vilevile uwaonye vijana wanaume wakuwe wenye utaratibu katika mambo yote. Na wewe unapaswa kuwa mufano katika matendo mema, ukionyesha ukweli na heshima katika mafundisho yako. Ufundishe maneno ya kweli watu wasiyoweza kubishia, hata wale wanaokupinga wapate haya kwa kukosewa na neno baya la kusema juu yetu. Sherti watumwa watii wabwana wao katika mambo yote na kuwapendeza, wakiepuka kubishana nao na kuiba vitu vyao. Lakini wajionyeshe kila mara kuwa waaminifu kamili, kusudi wapate kuheshimisha mafundisho juu ya Mungu Mwokozi wetu katika mambo yote. Kwa maana neema ya Mungu inayoleta wokovu kwa watu wote imeonekana waziwazi. Neema hii inatufundisha kwamba tuache uovu na tamaa za dunia, na kuishi katika dunia hii ya sasa katika ukadirifu, katika haki na kushikamana na ibada. Na hivi tutaishi tukingojea ule uheri tunaoutumainia, wakati utukufu wa Mungu wetu Mukubwa na Mwokozi wetu Yesu Kristo utakapotokea. Yeye alijitoa mwenyewe kwa ajili yetu, kusudi atukomboe toka uovu wote na kututakasa tupate kuwa watu wake wa pekee, watu wanaokuwa na hamu ya kufanya kazi nzuri. Haya ndiyo maneno unayopaswa kufundisha, ukiwaonya watu na kuwakaripia kwa mamlaka yote. Usijiachilie kuzarauliwa na mutu yeyote. Uwakumbushe watu wajinyenyekeze mbele ya watawala na wakubwa. Wanapaswa kuwatii na kuwa tayari kwa kufanya kila tendo zuri. Uwaambie wasiseme mabaya juu ya mutu, lakini wakuwe wenye kupenda amani na wema, na wenye kuonyesha upole mbele ya kila mutu. Kwa maana zamani sisi vilevile tulikuwa wajinga, waasi na wapotovu. Tulikuwa tumetawaliwa na kila namna ya tamaa mbaya na ya vitu mbalimbali vilivyotuvuta sana. Tuliishi katika uovu na wivu, tuliwachukiza watu nao walituchukia. Lakini wakati Mungu Mwokozi wetu alipoonyesha wema wake na upendo wake kwa watu, alituokoa sisi. Hakufanya vile kwa sababu ya matendo yetu ya haki, lakini alituokoa kwa sababu ya huruma yake kwa njia ya Roho Mutakatifu aliyetuwezesha kuzaliwa mara ya pili na kuwa na maisha mapya kwa kutusafisha kwa maji. Kwa maana Mungu amemimia Roho Mutakatifu kwa uwingi juu yetu kwa njia ya Yesu Kristo Mwokozi wetu. Ilifanyika vile, kusudi kwa neema yake tupate kuhesabiwa haki mbele ya Mungu na kuupata uzima wa milele tunaotumainia. Neno hilo ni la kuaminiwa. Ninataka uyatilie maneno hayo mukazo, kusudi watu walioamini Mungu wajitolee kwa kuzidi kutenda mema. Jambo hilo ni zuri na lenye mafaa kwa watu. Lakini uepuke mabishano ya upumbafu, hadisi za vizazi vya babu, na magomvi pamoja na mapingano juu ya Sheria, kwa sababu mambo hayo hayana mafaa, nayo ni ya bure. Ujiepushe na mutu anayeleta matengano unapokwisha kumwonya mara mbili. Kwa maana unajua kwamba mutu kama huyo amepotoka, na zambi zake zinamuhukumu yeye mwenyewe. Wakati nitakapokutumia Artema au Tikiko, ufanye bidii sana kuja kukutana nami kule Nikopoli, kwa maana nimekusudia kukaa kule wakati wa baridi kali. Ujikaze upate kumusafirisha vizuri mwanasheria Zenasi pamoja na Apolo, kusudi wasikose kitu chochote wanachohitaji katika safari yao. Inafaa watu wetu vilevile wajifunze kuzidi kutenda mema kusudi wapate kutoa musaada kwa ajili ya mahitaji ya kweli. Na hivi maisha yao yatakuwa yenye mafaa. Watu wote wanaokuwa pamoja nami wanakusalimia. Unisalimie wapendwa wetu katika imani. Ninawatakia ninyi wote neema kutoka kwa Mungu. Barua hii inatoka kwangu mimi Paulo, mufungwa kwa ajili ya Yesu Kristo, na kwa ndugu yetu Timoteo. Tunakuandikia wewe Filemono, mupendwa wetu na mwenzetu wa kazi, na kanisa linalokusanyika katika nyumba yako, na dada yetu Apia na Arkipo mupiganaji mwenzetu wa vita. Tunawatakia neema na amani toka kwa Mungu Baba yetu na Bwana wetu Yesu Kristo. Ninamushukuru Mungu wangu siku zote nikikukumbuka wewe Filemono katika maombi yangu. Kwa maana ninasikia namna unavyomwamini Bwana Yesu na namna unavyowapenda watu wote wa Mungu. Ninamwomba Mungu kwamba ushirika wa imani yako uzae matunda, na kwa njia hiyo upate kujua mema yote tunayokuwa nayo katika kuungana kwetu na Kristo. Ndugu, upendo wako umenifurahisha sana na kunifariji, kwa maana umetuliza mioyo ya watu wa Mungu. Kwa sababu hii, ingawa ninakuwa na mamlaka niliyopewa na Kristo kukuagiza neno unalopaswa kufanya, lakini kwa ajili ya upendo, ninapendelea kukusihi, mimi Paulo ninayekuwa muzee, na zaidi sasa ninakuwa mufungwa kwa ajili ya Yesu Kristo. Ninakusihi kwa ajili ya mutoto wangu Onesimo, niliyemuzaa katika imani nikiwa katika kifungo. Zamani yeye hakukufalia kitu, lakini sasa atakufalia wewe na mimi vilevile. Sasa ninamurudisha kwako, naye ni kama moyo wangu mimi mwenyewe. Ningalipenda Onesimo abakie pamoja nami kwa kunisaidia pahali pako wakati ninapokuwa mufungwa kwa sababu ya Habari Njema. Lakini sikutaka kufanya kitu chochote pasipo shauri lako. Wala sikutaka kukulazimisha unitendee mema; lakini ningetaka uyatende kwa mapenzi yako mwenyewe. Labda hii ndiyo sababu Onesimo aliachana nawe kwa muda, kusudi upate tena kuwa naye siku zote. Kwa sababu sasa yeye si kama vile mutumwa tu, lakini amekuwa bora zaidi kuliko mutumwa: yeye ni ndugu mupendwa. Mimi ninamupenda sana, nawe utamupenda zaidi sana, kwanza kama vile mutumwa, tena kama vile ndugu katika Bwana. Basi kama unaendelea kunihesabu kuwa mwenzako, umupokee kama vile ungenipokea mimi mwenyewe. Kama alikukosea au kama yuko na deni yako ya kitu chochote, unidai mimi. Mimi Paulo ninaandika kwa mukono wangu mwenyewe maneno haya: nitakulipa. (Sitaki kusema kwamba maisha yako ni deni unalokuwa nalo kwangu.) Ndiyo, ndugu yangu, ninakusihi unisaidie kwa njia hii kwa ajili ya Bwana, unitulize moyo kama vile ndugu katika Kristo. Ninapokuandikia, nina uhakika kwamba utanisikia na hata utafanya zaidi kuliko vile nilivyosema. Lakini pamoja na maneno haya, unitayarishie vilevile pahali pa kukaa, maana ninatumaini kwamba Mungu atajibu maombi yenu, na kunijalia nipate kurudishwa tena kwenu. Epafra, mufungwa mwenzangu, kwa ajili ya Yesu Kristo, anakusalimia. Vilevile Marko, Aristarko, Dema na Luka, wafanya kazi wenzangu, wanakusalimia. Ninawatakia ninyi wote neema kutoka kwa Bwana wetu Yesu Kristo. Zamani Mungu alisema na babu zetu kwa njia ya manabii, mara nyingi na kwa namna nyingi. Lakini kwa siku hizi za mwisho amesema nasi kwa njia ya Mwana wake. Mungu alimuweka kuwa murizi wa vitu vyote, na ambaye kwa njia yake aliumba ulimwengu wote. Yeye ni kitambulisho cha mwangaza wa utukufu wa Mungu, kwa maana yeye ni mufano kamili pahali ya Mungu mwenyewe, na kwa uwezo wa neno lake analinda vitu vyote. Naye alipokwisha kuwatakasa watu toka katika zambi zao, aliikaa na mamlaka katika mbingu kwa kuume kwa Mungu Mwenye Uwezo wote. Mwana amepata kuwa mukubwa kupita wamalaika kufuatana na lile jina alilopewa na Mungu, linalokuwa tukufu kuliko jina lao. Kwa maana Mungu hakumwambia hata mara moja mumoja wa wamalaika wake hivi: “Wewe ni mwana wangu, mimi leo nimekuwa baba yako.” Wala hakusema maneno haya juu ya malaika yeyote: “Mimi nitakuwa Baba yake, naye atakuwa Mwana wangu.” Na tena wakati Mungu alipomutuma muzaliwa wake wa kwanza katika dunia, alisema: “Wamalaika wote wa Mungu wanapaswa kumwabudu.” Lakini juu ya wamalaika, Mungu alisema: “Mungu anawafanya wamalaika wake kuwa kama upepo. Anawafanya hao watumishi wake kuwa kama ndimi za moto.” Lakini juu ya Mwana, Mungu alisema: “Kiti chako cha kifalme, Ee Mungu, kitadumu hata milele. Unatawala ufalme wako kwa haki. Unapenda haki na kuchukia uovu. Ni kwa hiyo Mungu, Mungu wako, amekusimika, akikupakaa mafuta, akikupatia heshima na kukuinua juu kuliko wenzako wote.” Vilevile Mungu alisema: “Wewe Bwana, kwa mwanzo uliumba dunia, mbingu ni kazi ya mikono yako. Vitatoweka lakini wewe utabaki. Vitachakaa kama nguo. Utavikunjakunja kama kanzu, navyo vitabadilishwa kama nguo. Lakini wewe utabaki sawasawa, na maisha yako hayatakuwa na mwisho.” Mungu hakumwambia hata mara moja mumoja wa wamalaika wake hivi: “Ikaa na mamlaka kwa kuume kwangu, mpaka nitakapowaweka waadui zako chini ya miguu yako.” Malaika ni nini, basi? Wao wote ni roho wanaomutumikia Mungu na wanaotumwa naye kwa ajili ya faida ya wale wanaopaswa kuokolewa. Kwa sababu hiyo, tunapaswa kushikamana zaidi na habari tuliyosikia, kusudi tusipotee mbali. Ujumbe wa Sheria uliotangazwa na malaika ulitimizwa, na hata kila mutu aliyekosa kuufuata na kuasi aliazibiwa sawa inavyostahili. Basi, namna gani sisi tutaponyoka azabu kama hatushuguliki na wokovu mukubwa kama huu? Ni Bwana mwenyewe aliyetangaza kwanza habari za wokovu huu, na wale waliomusikia walihakikisha kwetu kwamba ni za kweli. Mungu vilevile alihakikisha ushuhuda wao kwa njia ya maajabu, ya miujiza mbalimbali, na ya vitambulisho, na kwa njia ya zawadi za Roho Mutakatifu alizowapa watu kama anavyopenda. Mungu hakuwapa wamalaika uwezo wa kutawala ulimwengu unaokuja, ndio ule tunaosema juu yake. Tena maneno haya yanahakikishwa na pahali pengine katika Maandiko Matakatifu: “Mutu ni nini hata umukumbuke, mwanadamu ni nini hata umushugulikie? Umemufanya kuwa mwenye cheo chini kidogo ya malaika. Umemujaza utukufu na heshima. Umemupa mamlaka juu ya vitu vyote.” Wakati inaposemwa ya kama Mungu amemupa mutu mamlaka juu ya vitu vyote, maana yake hakuacha hata kitu kimoja. Ingawa hivi, hata sasa hatuoni kwamba amepewa mamlaka juu ya vitu vyote. Lakini mambo tunayoona ndiyo haya: Yesu alifanywa kuwa mwenye cheo chini kidogo ya malaika kusudi kwa neema ya Mungu, Yesu akufe kwa ajili ya watu wote. Na sasa kwa njia ya kile kifo kilichomufikia, amepata utukufu na heshima. Kwa hiyo ilifaa kwamba Mungu aliyeumba vitu vyote na kuvilinda imara, amufanye Yesu kuwa mukamilifu kwa njia ya mateso, kusudi awalete watoto wengi kuwa washiriki wa utukufu wa Mungu. Kwa maana Yesu ndiye anayewaongoza watu wapate kuokoka. Yeye anawatakasa watu toka katika zambi, na wale wanaotakaswa naye, wote ni watoto wa Baba mumoja. Ni kwa sababu hiyo Yesu hasikii haya ya kuwaita wandugu zake. Kwa maana anasema: “Ee Mungu, nitatangaza jina lako kwa wandugu zangu, nitakusifu katikati ya mukutano.” Tena anasema: “Nitamutumainia Mungu.” Na tena anasema: “Mimi ni hapa pamoja na watoto Mungu alionipatia.” Basi kwa kuwa hao watoto ni wanadamu, wenye mwili na damu, Yesu vilevile alitwaa ile hali ya mwanadamu. Alifanya hivi kusudi kwa njia ya kufa kwake amwangamize Shetani aliyekuwa na uwezo wa kuleta lufu. Vilevile aliwafungua wale wote walioishi kama watumwa katika maisha yao yote kwa sababu ya kuogopa lufu. Kwa maana hakika hakukuja kuwasaidia wamalaika, lakini alikuja kuwasaidia wazao wa Abrahamu. Kwa hiyo ilimupasa afanane na wandugu zake katika mambo yote, kusudi apate kuwa Kuhani Mukubwa anayekuwa mwenye huruma na mwaminifu katika kazi yake mbele ya Mungu, na kwa njia hiyo zambi za watu zisamehewe. Na kwa sababu yeye mwenyewe alijaribiwa na kuteswa, anaweza kuwasaidia wale wanaojaribiwa. Kwa sababu hiyo, wandugu zangu, ninyi ambao mumeitwa na Mungu na kuwa watu wake kama vile sisi, mufikiri sana juu ya Yesu, anayekuwa mutume na Kuhani Mukubwa wa imani tunayotangaza. Yeye alikuwa mwaminifu mbele ya Mungu aliyemusimika kwa kazi ile, sawa vile Musa alivyokuwa mutumishi mwaminifu katika kazi ya nyumba yote ya Mungu. Mujengaji wa nyumba anaheshimiwa zaidi kuliko nyumba yenyewe. Hivi vilevile Yesu anastahili kupewa heshima kubwa zaidi kuliko Musa. Ni kweli kila nyumba inajengwa na mutu, lakini Mungu ndiye aliyejenga vitu vyote. Musa alikuwa mutumishi mwaminifu katika nyumba yote ya Mungu, kusudi ashuhudie maneno ambayo Mungu angesema nyuma. Lakini Kristo ni mwaminifu kama Mwana anayesimamia nyumba ya Mungu. Na sisi ndio nyumba ile, kama tukiendelea kuwa na uhodari na kuaminia kupata mambo tunayotumainia. Kwa hiyo, kama vile Roho Mutakatifu anavyosema: “Leo ikiwa munasikiliza sauti ya Mungu, musifanye mioyo yenu kuwa migumu kama babu zenu walivyofanya wakati walipomwasi Mungu, sawa siku ile walipomupima katika jangwa. Kule babu zenu walinipima na kunijaribia, ingawa walikuwa wameona yote niliyotenda kwa muda wa miaka makumi ine. Kwa sababu ile nilikasirikia kizazi chao, na kusema: Watu hao wanapotoka siku zote. Nao hawafuati njia zangu. Basi nikaapa kwa kasirani kwamba hawataingia kwenye mapumziko niliyowatayarishia!” Basi wandugu zangu, muangalie vizuri, kati yenu kusikuwe mutu mumoja mwenye moyo mubaya wa kutokuamini, aliyefikia hata kujitenga mbali na Mungu Mwenye Uzima. Lakini muonyane kila siku kwa muda wote ambao lile neno “leo” linalotajwa lingali linatuelekea kusudi hata mumoja wenu asikuwe mugumu kwa kudanganywa na zambi. Kwa maana sisi wote tunaishi katika ushirika na Kristo ikiwa tunachunga mpaka mwisho lile tumaini tulilopata kwa mwanzo. Maandiko Matakatifu yanasema: “Leo ikiwa munasikiliza sauti ya Mungu, musifanye mioyo yenu kuwa migumu kama babu zenu walivyofanya wakati walipomwasi Mungu.” Ni watu gani waliosikia maneno ya Mungu na kumwasi? Si wale wote walioongozwa na Musa toka katika inchi ya Misri? Tena, ni watu gani waliomukasirikisha Mungu kwa muda wa miaka makumi ine? Si wale wote waliofanya zambi wakaanguka na kufa katika jangwa? Tena ni watu gani Mungu aliowaapia kwamba hawataingia kwenye mapumziko aliyowatayarishia? Si wale waliokataa kumutii? Basi tunaona kwamba hawakuweza kuingia kwenye mapumziko yale kwa sababu ya kutokuamini kwao. Basi kwa kuwa tungali na ahadi ya kuingia kwenye mapumziko yale, basi tufanye angalisho kusudi katikati yenu kusikuwe hata mutu mumoja atakayekosa kuingia. Kwa maana sisi vilevile tumehubiriwa Habari Njema kama vile watu wale. Walisikia habari lakini haikuwafalia kitu, kwa maana wale walioisikia hawakuipokea kwa imani. Lakini sasa sisi tulioamini, tutaingia kwenye mapumziko ambayo Mungu alitaja aliposema: “Halafu nikaapa kwa kasirani kwamba hawataingia hata kidogo kwenye mapumziko niliyowatayarishia!” Mungu alisema vile ingawa alikuwa amemaliza kazi zake tangu pale alipoumba dunia. Kwa maana imesemwa pahali fulani katika Maandiko Matakatifu juu ya siku ya saba: “Siku ya saba, Mungu akapumzika kwa maana alikuwa amemaliza kazi zake zote.” Na tena, katika Maandiko tuliyotaja hapa juu, Mungu anasema: “Hawataingia hata kidogo kwenye mapumziko niliyowatayarishia.” Wale waliokuwa wa kwanza kuhubiriwa Habari Njema hawakuingia kwenye mapumziko yale kwa sababu ya kutokuamini kwao. Ingawa vile ingali inawezekana kwa wengine kuingia. Kwa sababu hii Mungu anaweka tena siku ingine inayoitwa “Leo”. Naye alisema juu ya siku ile nyuma ya miaka mingi kwa njia ya Daudi, kufuatana na Maandiko haya yaliyokwisha kutajwa mbele: “Leo kama munasikiliza sauti ya Mungu musifanye mioyo yenu kuwa migumu.” Kwa maana kama Yoshua angekuwa amewafikisha watu kwenye mapumziko, Mungu hangesema tena nyuma ya pale juu ya siku ingine. Kwa hiyo kungali mapumziko ambayo Mungu anawatayarishia watu wake. Kwa maana yule anayeingia kwenye mapumziko anayotayarisha, anapumzika kwa kuwa amemaliza kazi zake zote kama vile Mungu alivyopumzika alipomaliza kazi zake. Basi tufanye bidii ya kuingia kwenye mapumziko yale, kusudi hata mutu mumoja asianguke sawa vile wale walioasi katika jangwa. Kwa maana Neno la Mungu ni lenye uzima, na lina nguvu; ni kali kupita upanga unaokata ngambo mbili. Linapenya hata linatenga moyo na roho na hata viungo na ubongo. Nalo linatambua nia na mawazo ya mutu. Hakuna kitu kinachoweza kufichwa mbele ya Mungu, lakini vitu vyote vinafunuliwa na viko wazi mbele ya macho yake, yeye tutakayemutolea hesabu ya maneno yetu. Basi, kwa kuwa tuko na Kuhani Mukubwa zaidi aliyeingia mbinguni, ndiye Yesu Mwana wa Mungu, tushikamane sana na imani tunayotangaza. Kwa maana tuko na Kuhani Mukubwa asiyekosa kujua mwenyewe uzaifu wetu. Maana yeye alijaribiwa katika njia zote sawasawa na sisi, lakini hakufanya zambi. Kwa sababu hii, tujongelee kwa uhodari kiti cha kifalme cha Mungu pahali anapowajalia watu neema kusudi apate kutuhurumia na kutujalia neema ya kutusaidia kwa wakati unaofaa. Kila Kuhani Mukubwa aliyechaguliwa kati ya watu amesimikwa kwa kumutumikia Mungu kwa ajili ya watu kusudi atolee matoleo na sadaka kwa ajili ya zambi. Kwa kuwa yeye mwenyewe ni muzaifu, anaweza kuwavumilia wale waliopotoka bila kujua. Na kwa sababu yeye mwenyewe ni muzaifu, anapaswa kutolea sadaka, si kwa sababu ya zambi za watu tu, lakini kwa sababu ya zambi zake mwenyewe vilevile. Hakuna mutu anayejipatia heshima hii ya kuwa Kuhani Mukubwa yeye mwenyewe. Lakini anapaswa kuitwa na Mungu, kama vile Haruni alivyoitwa. Hivi vilevile, Kristo hakujipatia yeye mwenyewe utukufu wa kuwa Kuhani Mukubwa, lakini ni Mungu ndiye aliyemwambia: “Wewe ni mwana wangu, mimi leo nimekuwa baba yako.” Vilevile alisema pahali pengine katika Maandiko: “Wewe ni kuhani hata milele kwa mufano wa Melkisedeki.” Wakati Yesu alipoishi katika dunia, aliomba na kusihi kwa malalamiko makubwa pamoja na kutoa machozi kwa Mungu ambaye angeweza kumwokoa toka katika kifo. Mungu alimusikia Yesu kwa sababu yeye alimuheshimu. Ijapokuwa alikuwa Mwana wa Mungu, alijifunza kutii kwa njia ya mateso yale aliyopata. Na alipokwisha kufanywa kuwa mukamilifu, akawaongoza watu wote wanaomutii wapate kuokolewa kwa milele. Basi, Mungu alitangaza kwamba yeye ni Kuhani Mukubwa kwa mufano wa Melkisedeki. Tuna maneno mengi ya kusema juu ya jambo hili, lakini ni vigumu kuyaeleza kwenu kwa sababu ninyi mumekuwa na masikio magumu. Kweli, kwa wakati huu, ninyi mungepaswa sasa kuwa walimu, lakini mungali munahitaji kufundishwa tena mafundisho ya mwanzo ya neno la Mungu. Mumegeuka tena wenye kuhitaji kunywa maziwa, wala si chakula kigumu. Kwa maana kila mutu anayeishi kwa kunyonya maziwa tu hawezi kufahamu mafundisho ya haki, maana yeye ni mutoto muchanga. Lakini chakula kigumu ni kwa ajili ya watu wazima, ndio wale waliozoeza mafikiri yao hata wapate kutambua mema na mabaya. Maana watu wanapokwisha kuangaziwa na ukweli wa Mungu na kuonja zawadi ya mbinguni, na kuishi katika ushirika na Roho Mutakatifu, wanapokwisha kuonja wema wa Neno la Mungu na nguvu za ulimwengu utakaokuja, kisha wakianguka, haiwezekani kuwarudisha hata wapate kugeuka mara ingine toka katika matendo yao mabaya. Kwa sababu wamemutundika wao wenyewe Mwana wa Mungu mara ya pili na kumupatisha haya mbele ya watu. Udongo unaonyeshewa na mvua mara kwa mara na kutoa mimea inayofaa kwa walimaji, unabarikiwa na Mungu. Lakini kama ukitoa miiba na magugu, udongo ule haufai kitu nao uko karibu ya kulaaniwa na Mungu, tena mwisho wake ni kuteketezwa. Lakini wapendwa wangu, ijapokuwa tunasema hivi, hatuna mashaka juu yenu, tukijua kwamba munafuata njia nzuri zaidi, ile ya wokovu wenu. Kwa maana Mungu ni mwenye haki. Yeye hatasahau kazi yenu na upendo mulioonyesha kwa ajili yake kwa namna mulivyowasaidia watu wake na munavyoendelea kuwasaidia. Lakini tunatamani sana kwamba kila mumoja kati yenu aendelee kuonyesha bidii ile mpaka mwisho, kusudi mambo yale munayotumainia yapate kutimizwa. Basi musigeuke kuwa wavivu, lakini mufuate mufano wa wale wanaoamini na kuvumilia. Kwa njia hiyo wanapokea yale Mungu aliyoahidi kuwapa. Wakati Mungu alipomupa Abrahamu ahadi, alifanya vilevile kiapo. Kwa sababu hakuna mutu mwingine mukubwa kuliko yeye kusudi ataje jina lake, akaapa kwa jina lake mwenyewe. Akasema: “Hakika nitakubariki sana na nitaongeza wazao wako.” Hivi kisha kungojea kwa uvumilivu, Abrahamu akapokea yale Mungu aliyomwahidi. Kwa maana watu wanapofanya kiapo, wanaapa kwa jina la mutu anayekuwa mukubwa kuliko wao wenyewe, nao uhakikisho wa kiapo kile unakomesha mabishano yote kati yao. Naye Mungu, kwa sababu alitaka kuonyesha wazi kwa wale watakaopokea ahadi kwamba yeye hawezi kubadilisha shauri lake hata kidogo, akaihakikisha kwa kiapo. Basi kuna mambo mawili, ahadi na kiapo, yasiyoweza kubadilika, na kuelekea hayo, Mungu hawezi kusema uongo. Kwa hivi, sisi tuliomukimbilia tunatiwa moyo sana na kushika kwa nguvu tumaini tulilowekewa. Tumaini hili linasimamisha imara na kulinda mioyo yetu kama vile nanga inavyosimamisha mashua imara. Nalo linapita katika pazia na kuingia katika Pahali Patakatifu Sana. Yesu alitangulia kuingia pahali pale kwa ajili yetu. Amekuwa Kuhani Mukubwa hata milele, kwa mufano wa Melkisedeki. Huyu Melkisedeki alikuwa mufalme wa Salemu na kuhani wa Mungu Mukubwa. Abrahamu alipokuwa akirudi toka katika vita nyuma ya kuwashinda wafalme wane, Melkisedeki alikutana naye na kumubariki, naye Abrahamu akamupa fungu moja la kumi la vitu vyote alivyoteka. Maana ya jina la Melkisedeki, kwanza ni “Mufalme wa haki,” tena ni mufalme wa Salemu, ni kusema “Mufalme wa amani.” Hakuna mambo yaliyoandikwa juu ya baba ya Melkisedeki, wala mama yake, wala majina ya babu zake. Tena, habari za kuzaliwa kwake na za kufa kwake hazijulikani. Anafanana na Mwana wa Mungu kwa kuwa yeye ni kuhani kwa milele. Basi muangalie namna mutu huyu alivyokuwa mukubwa, hata babu yetu mukubwa Abrahamu alimupa fungu moja la kumi la vitu vyote alivyoteka katika vita. Wazao wa Lawi wanaopewa kazi ya ukuhani wanaamriwa na Sheria kukongoa fungu moja la kumi la mapato toka kwa wandugu zao Waisraeli, ijapokuwa wao vilevile ni wa uzao wa Abrahamu. Lakini huyu Melkisedeki asiyekuwa wa uzao wa Lawi, alipokea fungu moja la kumi la vitu toka kwa Abrahamu. Na zaidi ya ile akamubariki Abrahamu, ambaye Mungu alikuwa amemutolea ahadi. Lakini bila shaka, yule anayebarikiwa ni mudogo kuliko yule anayebariki. Wale makuhani wanaopokea fungu la kumi ni watu wanaokufa; lakini Melkisedeki aliyepokea fungu la kumi anashuhudiwa kwamba anaishi. Basi tunaweza kusema hivi: wakati Abrahamu alipotoa fungu la kumi la mali yake, Lawi vilevile alilitoa kupitia yeye. Kwa maana ingawa Lawi alikuwa hajazaliwa bado, alikuwa yuko ndani ya damu ya babu yake Abrahamu, wakati Melkisedeki alipokutana naye. Ukuhani ndio ulikuwa musingi wa Sheria iliyotolewa kwa Waisraeli. Basi ikiwa ukamilifu ulipatikana kwa njia ya kazi ya ukuhani wa uzao wa Lawi, hakungekuwa tena lazima kutokee kuhani mwingine anayekuwa sawa na Melkisedeki, kwa pahali pa kuhani anayekuwa sawa na Haruni. Kwa maana wakati ukuhani unapobadilika, Sheria nayo inapaswa kubadilika vilevile. Naye Bwana wetu ambaye maneno haya yanamwelekea, alikuwa mutu wa kabila lingine, wala hakuna hata mutu mumoja wa kabila lake aliyefanya kazi ya ukuhani kwenye mazabahu. Kwa maana inajulikana wazi kwamba Bwana wetu alitoka katika kabila la Yuda, na juu ya kabila lile Musa hakusema hata neno moja linaloelekea ukuhani. Tena jambo hili linaloonyesha wazi zaidi maneno haya: kumetokea kuhani mwingine anayefanana na Melkisedeki. Huyu mwingine hakuwekwa kuwa kuhani kwa amri ya kimutu kufuatana na ukoo wake, lakini kufuatana na uwezo wa uzima usiokuwa na mwisho. Maana Maandiko Matakatifu yanashuhudia: “Wewe ni kuhani kwa milele kwa mufano wa Melkisedeki.” Kwa hiyo, ile amri ya zamani imevunjwa, kwa sababu ilikuwa zaifu nayo haikufaa kitu, kwa maana Sheria ya Musa haikuleta ukamilifu. Lakini sasa kumeletwa tumaini nzuri zaidi, na kwa njia ya tumaini hili tunaweza kumukaribia Mungu. Zaidi ya hii, mambo yale yalifanyika kufuatana na kiapo cha Mungu. Wale makuhani wengine wa uzao wa Lawi waliwekwa kwa kazi yao pasipo kiapo. Lakini Yesu amewekwa kuwa kuhani kwa njia ya kiapo, wakati Mungu alipomwambia: “Bwana ameapa, naye hatageuka: ‘Wewe ni kuhani kwa milele.’ ” Kwa sababu ya kiapo hiki, Yesu amekuwa kihakikisho kwetu cha agano linalokuwa zuri zaidi. Kuna tofauti ingine vilevile: wale makuhani wengine walipaswa kuwa wengi, kwa sababu walikuwa wakikufa hawakuweza kuendelea na kudumu katika kazi yao. Lakini Yesu hawezi kukombolewa kwa kazi yake ya ukuhani, kwa sababu yeye anaishi kwa milele. Ni kwa sababu hii anaweza kuwaokoa kabisa wao wanaokuja kwa Mungu kwa njia yake, kwa maana yeye anaishi siku zote kusudi akuwe mwombezi mbele ya Mungu. Basi Yesu ndiye Kuhani Mukubwa anayefaa kwa ajili yetu. Yeye ni mutakatifu, hana kosa wala alama ya uchafu. Ametengwa mbali na wenye zambi, naye amenyanyuliwa juu sana mbinguni. Yeye hahitaji kutoa sadaka kila siku kama vile Makuhani wengine Wakubwa, kwanza kwa ajili ya zambi zake mwenyewe na kisha kwa ajili ya zambi za watu. Kwa maana amefanya vile mara moja tu wakati alipojitoa mwenyewe kufa. Sheria ya Musa inawaweka watu wenye uzaifu kuwa Makuhani Wakubwa, lakini kufuatana na kiapo kilichokuja nyuma ya Sheria ile, Mwana anayekuwa mukamilifu kwa milele aliwekwa kuwa Kuhani Mukubwa. Jambo la lazima sana katika maneno tunayosema sasa ni hili. Tuko na Mukubwa wa namna ile, anayeikaa na mamlaka katika mbingu kwa kuume kwa Mwenyezi Mungu. Yeye anafanya kazi ya Kuhani Mukubwa katika Pahali Patakatifu Sana, maana yake katika hema ya kweli iliyosimikwa na Bwana, wala si mutu. Kila Kuhani Mukubwa anawekwa kusudi afanye kazi ya kutoa sadaka na matoleo. Kufuatana na hiyo, ilimupasa Kuhani wetu Mukubwa Kristo akuwe na kitu cha kutoa vilevile. Kama Kristo angekuwa katika dunia, asingekuwa kuhani hata kidogo, kwa sababu kuko makuhani wanaotoa sadaka kufuatana na maagizo ya Sheria. Kazi wale makuhani wanayofanya ni mufano na kitambulisho kinachoonyesha jinsi mambo kamili yanavyopitika mbinguni. Maneno hayo yanalingana na yale yaliyomutokea Musa. Wakati Musa alipokuwa karibu ya kujenga Hema, Mungu alimwambia: “Ufanye angalisho kusudi upate kutengeneza kila kitu kufuatana na mufano niliokuonyesha kwa mulima.” Lakini sasa Yesu amepewa kazi inayokuwa bora zaidi kuliko kazi ya wale makuhani, kwa maana yeye ni mupatanishi wa agano linalokuwa zuri zaidi. Sherti za agano lile zinasimamia juu ya ahadi ya Mungu inayokuwa bora zaidi. Kama lile agano la kwanza lingekuwa kamilifu, haingekuwa lazima likombolewe na la pili. Lakini Mungu aliwaonya watu wake, akisema: “Katika siku zinazokuja, nitafanya agano jipya na watu wa ufalme wa Israeli na wa Yuda. Ni Bwana anayesema hivyo. Agano lile halitakuwa sawa na lile nililofanya na babu zao siku nilipowakamatia kwenye mukono na kuwaondoa toka inchi ya Misri. Kwa sababu hawakushika lile agano, kwa hiyo vilevile sikuwashugulikia. Ni Bwana wetu Mungu anayesema hivyo. Sasa hili ndilo agano nitakalofanya na watu wa ufalme wa Israeli katika siku zile: nitawawezesha kuchunga sheria zangu ndani ya mafikiri yao, nikiziandika ndani ya mioyo yao. Ni Bwana wetu Mungu anayesema hivyo. Nitakuwa Mungu wao, nao watakuwa watu wangu. Hakutakuwa tena atakayefundisha mwanainchi mwenzake, au kumwambia ndugu yake: ‘Umujue Bwana.’ Kwa maana watu wote watanijua, tangu mudogo mpaka mukubwa. Mimi nitawasamehe maovu yao, wala sitakumbuka tena zambi zao.” Mungu alipotangaza hilo agano kuwa “jipya”, jambo hilo lilisababisha lile la kwanza kuwa la zamani na lenye kuchakaa. Na kitu chochote kikiwa cha zamani na chenye kuchakaa kinafikia wakati wa kutoweka. Katika agano la kwanza wanasema juu ya kanuni za ibada na juu ya nafasi ya kuabudia iliyojengwa na watu. Kufuatana na ile, kulikuwa Hema iliyosimikwa. Chumba chake cha kwanza kiliitwa Pahali Patakatifu. Ndani ya chumba kile kulikuwa kinara cha kuwekea taa, meza na mikate iliyotolewa kwa Mungu. Na nyuma ya pazia lililotenga kile chumba cha kwanza, kulikuwa chumba kingine kilichoitwa Pahali Patakatifu Sana. Ndani ya chumba kile kulikuwa chombo cha kufukizia ubani, kilichotengenezwa na zahabu. Na kulikuwa vilevile Sanduku la Agano lililopakaliwa zahabu pande zote. Ndani ya sanduku lile kulikuwa kopo la zahabu lenye mana, na fimbo ya Haruni iliyoota vichipukizi juu yake. Kulikuwa vilevile vibao vya mawe vyenye Maandiko ya Agano la Mungu. Na juu ya lile sanduku kulikuwa sanamu mbili za makerubi zilizoonyesha utukufu wa Mungu. Mabawa yao yalikuwa yakinyooshwa juu ya kiti cha rehema. Lakini sasa si wakati wa kueleza mambo hayo yote moja kwa moja. Ni hivi ndivyo walivyopanga vitu vile vyote. Halafu makuhani waliingia kila siku katika kile chumba cha kwanza kwa kufanya kazi za ibada. Lakini ni Kuhani Mukubwa peke yake ndiye aliyeingia katika kile chumba cha pili mara moja tu kila mwaka. Naye alipaswa kupeleka mule damu ya nyama anayotoa sadaka kwa ajili ya zambi zake mwenyewe na kwa ajili ya zambi watu walizofanya kwa kutokujua. Hivi Roho Mutakatifu alikuwa akionyesha kwamba njia ya kuingia katika Pahali Patakatifu Sana ilikuwa bado kufunguliwa kwa wakati wote ile Hema ya kwanza ilipokuwa ingali ikisimikwa. Huo ni mufano wa wakati wa sasa unaoonyesha kwamba matoleo na sadaka zinazotolewa kwa Mungu haziwezi kumufanya yule anayeabudu kuwa na moyo mukamilifu. Hizo ni kanuni za kimutu zinazoelekea vyakula na vinywaji pamoja na desturi mbalimbali za utakaso za kidini. Nazo zinaamuriwa kushikwa mpaka upate kutimia wakati wa kutengeneza vitu vyote upya. Lakini Kristo alikuja kuwa Kuhani Mukubwa anayeshugulika na mambo mema ambayo sasa yamekwisha kutokea. Yeye alipita katika hema inayokuwa bora zaidi na kamilifu. Hema hii haikutengenezwa na watu, maana yake si ya dunia hii. Aliingia mara moja tu katika Pahali Patakatifu Sana. Naye hakupeleka mule sadaka ya damu ya mbuzi na ya ngombe, lakini alipeleka damu yake mwenyewe. Na kwa njia ile akatukomboa kwa milele. Watu waliohesabiwa kuwa wachafu kufuatana na desturi, walitakaswa uchafu wao wa kimwili kwa njia ya kunyunyizwa damu ya mbuzi na ya ngombe pamoja na majivu ya ngombe aliyeteketezwa kwa moto. Ikiwa ni hivi, damu ya Kristo haitakuwa na uwezo zaidi wa kututakasa? Kwa maana kwa njia ya Roho anayeishi kwa milele, Kristo alijitoa mwenyewe kwa Mungu kuwa sadaka kamilifu. Nayo damu yake ikazitakasa zamiri zetu toka katika matendo yasiyofaa, kusudi tupate kumutumikia Mungu Mwenye Uzima. Kwa sababu hii, Kristo ni mupatanishi wa agano jipya. Kwa njia ya kufa kwake aliwakomboa watu toka katika makosa waliyofanya chini ya uongozi wa agano la kwanza, kusudi wale walioalikwa na Mungu wapate kupokea urizi wa milele aliowaahidia. Katika mambo yenye kuelekea agano la urizi, ni lazima kuhakikisha kwamba yule aliyelifanya amekwisha kufa. Agano kama hili linatimizwa nyuma ya kifo cha yule aliyelifanya, lakini si wakati angali muzima. Kwa sababu hii, hata lile agano la kwanza halikuwekwa pasipo kumwangika kwa damu. Kwa maana, kwanza Musa aliwatangazia watu wote amri zote za Sheria. Kisha akatwaa damu ya ngombe pamoja na maji, naye akavinyunyiza juu ya kitabu cha Sheria na juu ya watu wote akitumia manyoya mekundu na vitawi vya muti wa hisopo. Naye akasema: “Hii ndiyo damu inayohakikisha agano lile Mungu analowaamuru kutii.” Musa akanyunyiza vilevile damu juu ya Hema na juu ya vyombo vyote vya ibada. Na kufuatana na Sheria, karibu vitu vyote vinatakaswa kwa damu, nazo zambi haziwezi kusamehewa pasipo kumwangwa kwa damu. Basi ilikuwa lazima vitu vile vinavyoonyesha mufano wa mambo yanayopitika katika mbingu vitakaswe kwa njia ile. Lakini mambo kamili ya mbinguni yanahitaji kutakaswa kwa sadaka inayokuwa bora zaidi. Kwa maana Kristo hakuingia katika Pahali Patakatifu palipojengwa na watu, panapokuwa tu mufano wa Pahali Patakatifu kamili, lakini aliingia katika mbingu yenyewe, pahali anaposimama sasa mbele ya Mungu kwa kututetea. Kuhani Mukubwa wa Wayuda anaingia katika Pahali Patakatifu Sana kila mwaka, akibeba damu ya nyama. Lakini Kristo hakuingia humo kusudi ajitoe mwenyewe sadaka mara nyingi. Ingekuwa hivi, ingemupasa ateswe mara nyingi tangu kuumbwa kwa dunia. Lakini sasa, wakati ukikaribia kwa mwisho, yeye alitokea mara moja tu kusudi awasamehe watu zambi kwa njia ya kujitoa mwenyewe sadaka. Kila mutu anapaswa kufa mara moja tu, na nyuma ya kufa, anahukumiwa na Mungu. Hivi vilevile Kristo naye alijitoa kufa mara moja kusudi aondoe zambi za watu wengi. Naye atarudi tena, si kwa ajili ya kuondoa zambi, lakini kwa kuwaokoa wale wanaomungojea. Sheria ya Kiyuda ni mufano wa mema yatakayotokea, lakini si kitambulisho kinachoonyesha mambo yale kamili. Kwa sababu hii Sheria haiwezi hata mara moja, kwa njia ya sadaka zinazotolewa mara nyingi kila mwaka, kuwafanya wakamilifu wale wanaomwendea Mungu. Wale wanaomwabudu Mungu kwa njia ile wangetakaswa kabisa kwa mara moja tu, nayo zamiri yao isingewahukumu tena hata kidogo juu ya zambi, basi sadaka zile hazingeacha kutolewa. Lakini kwa njia ya sadaka zile, watu wanakumbushwa zambi zao kila mwaka, kwa sababu damu ya ngombe na ya mbuzi haiwezi kuondoa zambi. Kwa sababu hii, wakati Kristo alipokuja katika dunia alisema: “Wewe haukutaka sadaka wala matoleo. Lakini umeniumbia mwili. Haukupendezwa na sadaka za kuteketezwa kwa moto wala sadaka za kusamehewa zambi. Halafu nikasema: ‘Niko hapa, ee Mungu, nimekuja kufanya mapenzi yako, kama ilivyoandikwa juu yangu katika kitabu cha Sheria.’ ” Kwanza Kristo alisema: “Haukutaka wala haukupendezwa na sadaka na matoleo, wala sadaka za kuteketezwa kwa moto wala sadaka za kusamehewa zambi.” (Alisema vile ingawa sadaka hizo zote zilitolewa kufuatana na maagizo ya Sheria.) Kisha akasema: “Mimi niko hapa, ee Mungu, nimekuja kufanya mapenzi yako.” Kwa hiyo Mungu ameondoa hizo sadaka zote za kwanza na kuzikomboa na Kristo mwenyewe kama sadaka. Na kwa sababu Yesu Kristo alifanya mapenzi ya Mungu, sisi tumetakaswa zambi kwa njia ya mwili wake alioutoa sadaka kwa mara moja tu. Kila kuhani anasimama mbele ya Mungu kila siku kwa kufanya ibada na kutoa sadaka za namna moja mara nyingi zisizoweza hata kidogo kuondoa zambi. Lakini Kristo yeye alitoa sadaka moja tu inayofaa kwa milele kwa ajili ya usamehe wa zambi. Na kisha akaikaa na mamlaka kwa kuume kwa Mungu. Na kule anangoja sasa mpaka waadui zake wote watiwe chini ya miguu yake. Kwa maana kwa njia ya sadaka moja aliyotoa, amewafanya wale aliowatakasa kuwa wakamilifu hata milele. Naye Roho Mutakatifu anatushuhudia mambo hayo vilevile. Kwanza anasema maneno haya: “Hili ndilo agano nitakalofanya nao nyuma ya siku zile. Ni Bwana wetu Mungu anayesema hivyo. Nitawawezesha kuchunga sheria zangu ndani ya mafikiri, nikiziandika ndani ya mioyo yao.” Naye anaongeza kusema: “Nami sitakumbuka tena zambi wala maovu yao.” Basi wakati zambi zinaposamehewa, hakuna tena hitaji la kutoa sadaka kwa ajili ya usamehe wa zambi. Basi wandugu, tuko na uhodari wa kuingia katika Pahali Patakatifu kwa njia ya damu ya Yesu. Yeye ametufungulia njia mupya ya uzima, inayopitia katika pazia, maana yake mwili wake mwenyewe. Sisi tuko na Kuhani Mukubwa anayesimamia nyumba yote ya Mungu. Basi tumwendee Mungu kwa moyo wa uaminifu, kwa imani kamilifu, kwa moyo uliosafishwa toka zamiri mbaya na mwili uliosafishwa na maji safi. Tuendelee kuchunga lile tumaini tuliloshuhudia bila kuchoka, kwa maana Mungu aliyetupatia ahadi ni mwaminifu. Tena tushugulikiane kusudi tupate kuvutana sisi kwa sisi kuwa na upendo na kufanya mema. Tusiache kukusanyika pamoja, kama vile wamoja wanavyozoea kufanya. Lakini tuonyane, na zaidi sana kufuatana na vile munavyoona kwamba Siku ya Bwana inakaribia. Kwa maana tukifanya zambi kwa makusudi tukisha kutambua waziwazi ukweli, hakuna tena sadaka ingine inayoweza kutolewa kwa ajili ya usamehe wa zambi zetu. Lakini inayobaki tu ni kungojea kwa woga hukumu na moto mukali wa Mungu utakaowateketeza waasi. Mutu yeyote aliyevunja Sheria ya Musa, aliuawa bila huruma kisha ushuhuda wa watu wawili au watatu. Basi munazania itakuwa namna gani? Hataazibiwa vikali zaidi yule anayemuzarau Mwana wa Mungu na kuihesabu kuwa bure damu ya agano la Mungu iliyomutakasa na kumutukana Roho wa neema? Kwa maana tunamujua yule aliyesema: “Ni kazi yangu kulipiza kisasi. Ni mimi nitakayelipiza.” Naye alisema tena: “Bwana atawahukumu watu wake.” Kuanguka katika mikono ya Mungu Mwenye Uzima ni jambo la kuogopa sana! Mukumbuke mambo yaliyowatokea katika siku zilizopita. Ninyi mulipokwisha kuangaziwa na Mungu, mulipita katika mateso mengi lakini mulivumilia. Kwa ngambo moja mulitukanwa na kuteswa waziwazi mbele ya watu. Na kwa ngambo ingine mulishirikiana na wale waliotendewa vibaya. Muliwahurumia wale waliokuwa katika kifungo, nanyi mulikubali kwa furaha kunyanganywa mali zenu, kwa sababu mulijua kwamba muko na mali inayokuwa bora zaidi na yenye kudumu. Basi musikate tumaini, kwa maana litawaletea zawadi kubwa. Munapaswa kuvumilia, kusudi mutimize mapenzi ya Mungu, na kuweza hivi kupewa kile mulichoahidiwa. Kwa maana, kama vile Maandiko haya Matakatifu yanavyosema: “Kunabaki wakati kidogo sana, yule anayepaswa kuja, afike wala hatakawia. Mwenye haki mbele yangu ataishi kwa njia ya imani. Lakini kama akirudi nyuma, sitapendezwa naye.” Lakini sisi si watu wenye kurudi nyuma na kupotea, lakini sisi ni watu wenye imani na wenye kuokoka. Kuwa na imani ni kuwa na uhakika juu ya mambo tunayotumainia, ni kusadiki kabisa mambo tusiyoyaona. Ni kwa sababu ya imani yao babu zetu wameshuhudiwa vizuri na Mungu. Kwa njia ya imani tunafahamu kwamba ulimwengu uliumbwa kwa amri ya Mungu, hata vitu vinavyoonekana, viliumbwa kutoka vile visivyoonekana. Kwa njia ya imani, Abeli alimutolea Mungu sadaka nzuri zaidi kuliko ile ya Kaina. Kwa ajili ya imani yake alihesabiwa na Mungu kuwa mwenye haki, kwa maana Mungu mwenyewe alikubali sadaka zake. Na kwa imani ile, ingawa Abeli amekwisha kufa, angali anasema. Kwa njia ya imani, Enoki alibebwa na Mungu toka katika dunia pasipo kufa. Naye hakuonekana tena, kwa sababu Mungu alimubeba mbinguni. Maana Maandiko Matakatifu yanasema kwamba mbele ya kubebwa kwake, Enoki alishuhudiwa kwamba alimupendeza Mungu. Basi pasipo imani, hakuna mutu anayeweza kumupendeza Mungu. Kwa maana mutu anayetaka kumwendea Mungu sherti aamini kwamba Mungu yuko, na kwamba anawapa zawadi wale wanaomutafuta. Kwa njia ya imani, Noa alionywa na Mungu juu ya mambo yatakayotokea, yale aliyokuwa hajayaona bado. Yeye alimutii Mungu na kujenga chombo kwa kujiokoa yeye mwenyewe pamoja na jamaa yake. Kutokana na hayo yote akahukumu dunia na kupokea haki inayopatikana kwa njia ya imani. Kwa njia ya imani, Abrahamu alitii wakati Mungu alipomwita na kwenda katika inchi ile Mungu aliyoahidi kumupatia kuwa urizi wake. Akaacha inchi yake pasipo kujua pahali anapokwenda. Kwa njia ya imani, aliishi kama vile mugeni katika inchi ile Mungu aliyomwahidi. Yeye alikuwa akiishi katika hema kama vile Isaka na Yakobo walivyoishi. Wao vilevile walishiriki pamoja naye ahadi ile ile ya Mungu. Kwa maana Abrahamu alitazamia kuona muji wenye musingi wa nguvu, muji ambao Mungu mwenyewe ndiye fundi aliyeuchapa na kuujenga. Kwa njia ya imani, Sara mwenyewe vilevile, ijapokuwa alikuwa muzee sana, alijaliwa uwezo wa kupata mimba kwa sababu aliamini kwamba Mungu atatimiza ahadi yake. Kwa sababu hiyo, kwa njia ya mutu mumoja aliyekuwa akingojea kufa, kukazaliwa wazao wengi sana kama nyota na kama muchanga unaokuwa kandokando ya bahari. Watu hawa wote walikufa katika imani pasipo kupokea mambo Mungu aliyoahidi. Lakini waliyaona kwa mbali na kuyafurahia, wakikubali kwamba walikuwa wageni na wasafiri katika dunia. Maana watu wanaosema maneno kama haya wanaonyesha wazi kwamba wanatafuta inchi yao wenyewe. Kama wangekumbuka inchi yao walioiacha zamani, wangeweza kupata namna ya kurudia kule. Lakini kwa hakika walitamani sana inchi inayokuwa bora zaidi, ndiyo inchi ya mbinguni. Kwa sababu hii Mungu hasikii haya kuitwa Mungu wao, maana amewatayarishia muji. Kwa njia ya imani, Abrahamu alimutoa Isaka kama vile sadaka wakati Mungu alipopima imani yake. Abrahamu alikubali kumutoa mwana wake wa pekee, ingawa ni yeye ndiye aliyekuwa amepewa ahadi na Mungu. Mungu alikuwa amemwambia: “Ni kwa njia ya Isaka utapata wazao watakaoitwa wako.” Abrahamu aliamini kwamba Mungu anaweza kumufufua Isaka na hivi akarudishiwa tena Isaka kama vile mwenye kufufuka. Kwa njia ya imani, Isaka aliwabariki Yakobo na Esau kuelekea mambo ya siku zitakazokuja. Kwa njia ya imani, Yakobo alipokuwa karibu kufa, alibariki kila mumoja wa wana wa Yosefu; akainama kwa kumwabudu Mungu akiegemea fimbo yake. Kwa njia ya imani, Yosefu alipokuwa karibu kufa, alisema juu ya habari za wakati Waisraeli watakapotoka katika inchi ya Misri, na kuwaagiza juu ya mifupa yake. Kwa njia ya imani wazazi wa Musa walimuficha kwa muda wa miezi mitatu nyuma ya kuzaliwa kwake. Kwa sababu waliona kwamba alikuwa mutoto mwenye sura nzuri, wala hawakuogopa amri ya mufalme. Kwa njia ya imani, Musa alipokuwa mutu muzima, alikataa kuitwa mwana wa binti wa mufalme wa Misri. Alifikiri kwamba ni afazali kuteswa pamoja na watu wa Mungu kuliko kujifurahisha katika zambi kwa muda mufupi. Aliona kwamba kupatishwa haya kwa ajili ya Kristo kuna faida kubwa zaidi kuliko kupata utajiri wote wa inchi ya Misri, maana alikuwa anatazamia kupokea zawadi yake. Kwa njia ya imani, Musa alitoka katika inchi ya Misri bila kuogopa kasirani ya mufalme. Na kama vile mutu mwenye kumwona Mungu asiyeonekana, yeye hakurudi nyuma. Kwa njia ya imani, alianzisha sikukuu ya Pasaka, na kuamuru damu inyunyizwe, kusudi malaika mwangamizaji asiwaue wazaliwa wa kwanza wanaume wa Waisraeli. Kwa njia ya imani, Waisraeli walivuka bahari Nyekundu kama vile ingekuwa katika inchi kavu. Lakini wakati Wamisri walipojaribu kufanya vile, walizama na kufa ndani ya maji. Kwa njia ya imani, ukuta uliozunguka muji Yeriko ulianguka wakati Waisraeli walipokwisha kuuzunguka kwa muda wa siku saba. Kwa njia ya imani, Rahaba, yule kahaba, hakuangamia pamoja na wale waliomwasi Mungu, kwa sababu aliwakaribisha wapelelezi kwa amani. Basi niseme nini tena? Maana wakati hauniruhusu kueleza habari juu ya Gideoni, Baraka, Samsoni, Yefuta, Daudi, Samweli na manabii. Kwa njia ya imani hawa walishinda inchi za wafalme, walitenda mambo ya haki na kupata yale Mungu aliyowaahidi. Walifunga vinywa vya simba, walizimisha moto mukali, waliponyoka kuuawa kwa upanga. Walikuwa wazaifu, lakini wakapata nguvu; walikuwa shujaa katika vita na kushinda majeshi ya kigeni. Kwa njia ya imani, wanawake wamoja walifufuliwa na kurudishiwa wale waliofiwa nao. Wengine waliteswa mpaka kufa, nao wakikataa kuachiliwa kusudi wapate ufufuko unaokuwa bora zaidi. Wengine walichekelewa na kupigwa fimbo, na wengine walifungwa minyororo na kutupwa katika kifungo. Wengine waliuawa kwa kutupiwa mawe, wengine walikatwa vipandevipande kwa misumeno, au kuuawa kwa upanga. Walitangatanga wakivaa ngozi za kondoo au za mbuzi, wakiishi katika umasikini, wakiteswa na kutendewa vibaya. Dunia haikustahili kuwa na watu kama hawa! Walitangatanga katika jangwa na katika milima, wakiishi katika mapango na mashimo ndani ya udongo. Watu hawa wote walishuhudiwa vizuri na Mungu kwamba wamemupendeza kwa njia ya imani yao. Lakini hawakupokea mambo yale Mungu aliyowaahidia, kwa maana Mungu alikuwa ametayarisha mambo mazuri zaidi kwa ajili yetu kusudi wao wenyewe wasipate kukamilishwa bila sisi vilevile. Nasi vilevile tunazungukwa na kundi kubwa kama lile la wale walioshuhudia imani yao. Basi tutupilie mbali vitu vyote vinavyotusonga, nazo zambi zinazotufunga upesi na tukimbie kwa juhudi sana katika mashindano tunayowekewa. Tukaze macho yetu kuelekea Yesu mwenye kuanzisha na kukamilisha imani yetu. Kwa sababu alijua furaha atakayopata nyuma, alivumilia kufa juu ya musalaba pasipo kuona haya, na sasa anaikaa na mamlaka kwa kuume kwa Mungu kwenye kiti cha kifalme cha Mungu. Kwa hiyo mumukumbuke yule aliyevumilia kutendewa na wenye zambi kwa chuki kubwa, kusudi musipate kuchoka wala kuregea. Kwa maana katika vita munayofanya kwa kushinda zambi, hamujapigana bado mpaka kufa. Na zaidi ya hii, mumesahau maonyo haya Mungu anayotoa kwenu kama wana wake? “Mwana wangu, usizarau azabu ya Bwana wala usiregee wakati anapokukaripia. Kwa maana, Bwana anamwazibu yule anayemupenda, yeye anamupiga kila mutu anayemukubali kuwa mutu wake.” Muvumilie maadibisho; kwa maana Mungu anawatendea ninyi kama wana wake. Tena, ni mwana gani asiyeazibiwa na baba yake? Ikiwa hamuadibishwi na Mungu sawa vile watoto wake wote wanavyoadibishwa, basi ninyi si wana wa kweli wa Mungu, ninyi ni wana haramu. Na ikiwa wababa zetu wa kimwili walituadibisha, nasi tuliwaheshimu, jambo hilo halionyeshi zaidi kwamba tunapaswa kumuheshimu Baba yetu wa kiroho na kupata kuishi? Wababa zetu wa kimwili walituadibisha kwa siku chache kufuatana na vile walivyoona kuwa vema. Lakini Mungu anatuadibisha kwa mafaa yetu kusudi tupate kushirikiana naye katika utakatifu wake. Maadibisho yoyote wakati yanapotolewa yanaonekana kama ni tendo la huzuni wala si la furaha. Lakini kwa mwisho yanawaletea wale waliofundishwa nayo, maisha ya amani na ya haki. Basi muitie tena nguvu mikono yenu inayopooza, nayo magoti yenu yanayoregea. Mujitengenezee njia zenye kunyooka, kusudi mwenye ulema wa miguu asiteguke, lakini apate kupona. Mujikaze kwa kuishi katika amani na watu wote na kuishi katika utakatifu, kwa sababu hakuna mutu asiyeishi katika hali hiyo atakayemwona Bwana. Muangalie vizuri, kusudi hata mutu mumoja asijikoseshe mwenyewe kupata neema ya Mungu, wala asikuwe sawa shina la mumea unaotoa matunda machungu na kuleta fujo kati yenu na kuambukiza watu wengi. Vilevile muangalie vizuri, kusudi hata mutu mumoja asikuwe mwasherati au mwenye kukufuru Mungu kama vile Esau aliyeuzisha haki yake ya muzaliwa wa kwanza kwa ajili ya chakula kidogo tu. Kama munavyojua, nyuma ya pale alikataliwa wakati alipotaka kupokea baraka toka kwa baba yake. Yeye hakukuwa tena na namna ya kugeuza tendo lake ijapokuwa alitafuta baraka ile kwa machozi. Ninyi hamujafikia kwenye kitu kinachoweza kuguswa kama vile Waisraeli walivyofikia kwenye mulima Sinai. Mulima ule uliwaka moto, ulifunikwa na giza nzito, nao ulikuwa na uvumi wa zoruba juu yake. Vilevile juu yake kulisikilika mulio wa baragumu na ngurumo ya sauti. Nao Waisraeli waliposikia sauti ile wakasihi wasiambiwe tena neno, kwa sababu hawakuweza kuvumilia agizo walilotolewa: “Hata nyama akigusa mulima anapaswa kuuawa kwa kutupiwa mawe.” Na mambo yale yaliyoonekana yalikuwa ya kuogopesha sana, hata Musa akasema: “Ninaogopa na kutetemeka!” Lakini ninyi mumefikia kwenye mulima Sayuni na kwenye muji wa Mungu Mwenye Uzima, ndio muji Yerusalema wa mbinguni, kunakokuwa maelfu na maelfu ya wamalaika. Lakini ninyi mumefikia kwenye mukutano wa furaha wa wazaliwa wa kwanza wa Mungu walioandikwa majina zao katika mbingu. Mumefikia vilevile karibu na Mungu, anayekuwa mwamuzi wa watu wote na kwenye nafsi kunapokuwa roho za watu wenye haki waliofanywa kuwa wakamilifu. Mumefikia karibu na Yesu anayekuwa mupatanishi wa agano jipya, na kwenye damu yake iliyomwangwa inayosema nasi maneno mema zaidi kuliko damu ya Abeli. Basi muangalie vizuri kusudi musikatae kumusikiliza yule anayesema nanyi. Wale waliokataa kusikiliza yule aliyewaonya hapa katika dunia hawakuponyoka azabu ya Mungu. Si jambo hilo linaonyesha wazi kwamba sisi hatutaweza kuponyoka kama tunamugeuzia mugongo yule anayetutolea maonyo kutoka mbinguni? Katika wakati ule sauti yake ilitetemesha dunia, lakini sasa ametuahidi hivi: “Nitatetemesha dunia mara moja tena, wala si dunia tu, lakini mbingu vilevile.” Neno hili “mara moja tena” linaonyesha kwamba vitu vilivyoumbwa vitatikiswa na kutoweka, kusudi vile visivyoweza kutikiswa vipate kudumu. Basi kwa kuwa tunakubaliwa kuwa washiriki wa ufalme usioweza kutikiswa, tukuwe watu wenye shukrani. Tuonyeshe shukrani ile kwa kumwabudu Mungu kwa njia inayomupendeza kwa heshima na woga, kwa maana Mungu wetu ni kama moto wenye kuteketeza. Muendelee kuishi katika upendo wa kindugu. Musisahau kuwakaribisha wageni, maana kwa kufanya hivi wamoja wamewakaribisha wamalaika pasipo kujua. Muwakumbuke wale wanaofungwa, mukijisikia sawa vile wenye kufungwa pamoja nao. Vilevile muwakumbuke wale wanaoteswa, mukijisikia sawa vile wenye kuteswa kama wao. Ndoa inapaswa kuheshimiwa na watu wote, mume na muke wake wanapaswa kujikinga na uchafu, kwa sababu Mungu atawahukumu wazinzi na waasherati. Musijiachilie kutawaliwa na tamaa ya mali katika maisha yenu, lakini mutoshelewe na vitu munavyokuwa navyo, kwa maana Mungu mwenyewe amesema: “Sitakusahau wala kukuachilia.” Kwa sababu hii tunaweza kusema kwa uhodari: “Bwana ndiye musaidizi wangu; sitaogopa kitu. Mwanadamu ataweza kunifanya nini?” Muwakumbuke waongozi wenu waliowatangazia neno la Mungu. Muangalie vizuri namna walivyoishi na kufa. Mufuate imani yao. Yesu Kristo ni yule yule, jana, leo na hata milele. Musidanganywe na mafundisho mengine ya kigeni ya kila namna. Kwa maana mioyo yetu inapaswa kutiwa nguvu kwa njia ya neema ya Mungu, wala si kwa njia ya kushika kanuni zinazoagizwa juu ya vyakula. Kanuni hizo haziwafalii kitu wale wanaozishika. Sisi tuko na mazabahu yetu, nao makuhani Wayuda wanaotumika katika Pahali Patakatifu hawana ruhusa ya kula sehemu ya vitu vinavyotolewa sadaka juu ya mazabahu ile. Kuhani Mukubwa anapeleka damu ya nyama ndani ya Pahali Patakatifu Sana kwa ajili ya kuitoa kuwa sadaka ya kusamehewa zambi lakini viungo vyote vya nyama wale vinateketezwa kwa moto mbali na kambi. Kwa sababu hii Yesu vilevile aliuawa mbali na muji kusudi awatakase watu wake kwa njia ya damu yake mwenyewe. Basi tumwendee mbali na kambi, tukikubali kuzarauliwa kama vile yeye alivyozarauliwa. Kwa maana hapa katika dunia hatuna muji unaodumu, lakini tunatazamia muji ule unaokuja. Basi kwa njia ya Yesu, tumutolee Mungu sadaka za kumusifu siku zote, maana yake kutangaza kwamba tunaaminia jina lake. Tena, musisahau kutenda mema na kusaidiana, maana sadaka za namna hii zinamupendeza Mungu. Mutii waongozi wenu na kushika maagizo yao. Kwa maana wao wanashugulika kila mara kwa ajili ya roho zenu, na wao wanapaswa kutoa habari ya kazi yao mbele ya Mungu. Kwa kufanya vile mutawaruhusu kufanya kazi yao kwa furaha wala si kwa huzuni, kwa maana haitawafalia kitu kama wakitumika katika huzuni. Muzidi kutuombea. Tuna uhakika kwamba tuko na zamiri safi, kwa maana tunataka kuwa na mwenendo mwema katika mambo yote. Ninawasihi sana kuomba Mungu, kusudi nipate kurudishwa kwenu upesi. Mungu wa amani, aliyemufufua Bwana wetu Yesu ambaye ni Muchungaji mukubwa wa kondoo kwa njia ya kumwanga damu yake inayohakikisha agano la milele, awakamilishe katika kila tendo jema kusudi mupate kutimiza mapenzi yake; yeye atimize ndani yetu yale yanayomupendeza, kwa njia ya Yesu Kristo. Yesu atukuzwe milele na milele. Amina. Wandugu, ninawasihi kupokea kwa uvumilivu haya maonyo ninayowatolea kwa maana nimewaandikia kwa kifupi. Ninapenda kuwajulisha kwamba ndugu yetu Timoteo amekwisha kufunguliwa. Kama akikuja upesi, nitafika kuwaona pamoja naye. Muwasalimie waongozi wenu wote na watu wote wa Mungu. Wandugu wa Italia wanawasalimia. Tunawatakia ninyi wote neema ya Mungu. Barua hii inatoka kwangu mimi Yakobo, mutumishi wa Mungu na wa Bwana Yesu Kristo. Ninawasalimia ninyi watu wa makabila kumi na mawili waliosambazwa katika dunia. Wandugu zangu, muhesabu kuwa ni jambo la furaha sana wakati munapopata majaribu ya namna mbalimbali, kwa maana munajua kwamba kupimwa kwa imani yenu kunawaletea uvumilivu. Lakini sherti uvumilivu ule utimize kazi yake, kusudi mupate kuwa wakamilifu na watimilifu wasiopungukiwa na kitu. Kama mumoja kati yenu akikosa kuwa na hekima, aiombe kwa Mungu ambaye atamupatia. Kwa maana Mungu anawapa watu wote bila upendeleo na kwa moyo mwema. Lakini inafaa aombe kwa imani pasipo kuwa na mashaka. Kwa maana mutu anayekuwa na mashaka anafanana na zoruba katika bahari inayosukumwa na upepo na kutupa maji huku na huko. Mutu wa namna hiyo asizani kwamba atapokea kitu chochote kutoka kwa Bwana, kwa sababu ni mutu wa nia mbili, na mwenye kugeukageuka katika mwenendo wake. Ndugu anayekuwa masikini afurahi kwa sababu Mungu anamupandisha, na ndugu anayekuwa tajiri afurahi kwa sababu Mungu anamushusha. Maana tajiri atatoweka kama maua ya pori. Jua linatokea na kwa joto kali linakausha mimea, nayo maua yake yanaanguka na uzuri wake wote unaharibika. Hivi ndivyo tajiri naye atakavyotoweka katika shuguli zake. Heri mutu yule anayevumilia wakati anapojaribiwa, kwa maana akiisha kushinda majaribu, atapokea ile taji ya uzima ambayo Mungu aliahidia wale wanaomupenda. Wakati mutu anapojaribiwa, asiseme hivi: “Ninajaribiwa na Mungu!” Kwa maana Mungu hawezi kujaribiwa na ubaya, wala yeye mwenyewe hawezi kumujaribu mutu. Lakini kila mutu anajaribiwa wakati anapovutwa na kudanganywa na tamaa yake mbaya mwenyewe. Halafu ile tamaa mbaya ikisha kukomaa, inazaa zambi, nayo zambi ikisha kukomaa inazaa lufu. Wandugu zangu wapendwa, musidanganyike! Kila zawadi nzuri na kila zawadi kamilifu inatoka juu kwa Mungu Baba aliyeumba miangaza yote inayokuwa katika mbingu. Mungu hawezi kubadilika wala kugeuka. Kwa mapenzi yake mwenyewe alitupatia sisi uzima kwa njia ya ujumbe wa kweli, kusudi tupate kuwa kama mavuno ya kwanza katikati ya viumbe vyake. Wandugu zangu wapendwa, mukumbuke neno hili: kila mutu anapaswa kuwa mwepesi kwa kusikia, lakini asikuwe mwepesi kwa kusema na kukasirika. Kwa maana mutu mwenye kasirani hawezi kutimiza mambo ya haki mbele ya Mungu. Kwa sababu hiyo, mutupilie mbali mambo yote machafu na matendo ya uovu yanayozidi. Mupokee kwa unyenyekevu neno lile lililopandwa ndani yenu na linaloweza kuwaokoa. Musijidanganye ninyi wenyewe kwa kusikiliza tu neno la Mungu, lakini mulitimize kwa matendo. Kwa maana mutu anayesikia neno tu pasipo kulitimiza, anafanana na mutu anayejiangalia sura yake mwenyewe katika kioo. Kisha kujiangalia, anajiendea, na mara moja anasahau namna anavyokuwa. Lakini mutu anayechunguza sheria kamilifu inayoweka watu huru na kuendelea kushikamana nayo, na si kuisikia tu na kisha kuisahau, lakini anaitimiza kabisa, mutu huyu atabarikiwa na Mungu katika shuguli zake. Kama mutu akizani kwamba yeye ni mutu wa dini naye hawezi kuzuiza ulimi wake, anajidanganya mwenyewe, nayo dini yake haina faida. Dini inayokuwa safi na bila kosa mbele ya Mungu Baba ndiyo hii: kushugulikia wayatima na wajane wanaoteswa, na kujilinda mwenyewe na uchafu wa dunia hii. Wandugu zangu, kufuatana na vile munavyomwamini Bwana wetu Yesu Kristo mwenye utukufu, musikuwe vilevile na upendeleo na watu. Kwa mufano: tajiri mumoja anayevaa pete ya zahabu na nguo nzuri anaingia katika nyumba yenu ya kuabudia. Na kisha kunaingia vilevile masikini anayevaa nguo zinazopasukapasuka. Halafu munaonyesha heshima kwa yule anayevaa vizuri na kumwambia: “Ikaa hapa kwenye nafasi nzuri.” Lakini munamwambia yule masikini: “We! Simama pale, au uikae hapa chini kwenye nafasi ya kuwekea miguu yangu.” Jambo hilo halionyeshi kwamba munafanya ubaguzi, na kwamba kwa kuamua vile munaongozwa na mawazo mabaya? Wandugu zangu wapenzi, musikilize: Mungu amewachagua wamasikini wa dunia hii kusudi wakuwe watajiri katika imani, nao wapokee Ufalme ule aliowaahidi wale wanaomupenda. Lakini ninyi munawazarau wamasikini! Watajiri si ndio wale wanaowagandamiza ninyi na kuwashitaki kwenye tribinali? Vilevile si wao ndio wanaotukana jina lile nzuri mulilopewa? Munafanya vizuri kama mukitimiza sheria hii ya kifalme inayopatikana katika Maandiko Matakatifu: “Umupende mwenzako kama unavyojipenda wewe mwenyewe.” Lakini kama mukifanya upendeleo, munafanya zambi, nanyi munahukumiwa na Sheria kwa sababu mumeivunja. Kwa maana mutu akivunja agizo moja tu la Sheria, yeye anavunja Sheria yote. Kwa maana yule aliyesema “Usizini”, ndiye aliyesema vilevile “Usiue”. Basi ikiwa wewe huzini lakini unaua, wewe unavunja Sheria. Basi museme na kutenda kama watu watakaohukumiwa kufuatana na sheria inayotuweka kuwa huru. Kwa sababu Mungu hatahurumia mutu yule asiyehurumia wengine. Lakini huruma ya Mungu itaishinda hukumu. Wandugu zangu, ni faida gani kama mutu akisema kwamba yuko na imani lakini haionyeshi kwa njia ya matendo mazuri? Ile imani itaweza kumwokoa? Kwa mufano: kaka au dada fulani akikosewa nguo au chakula, itakuwa na faida gani, kama mumoja wenu anamwambia: “Mwende vizuri, mukaote moto na kushiba,” lakini hamusaidii na kitu chochote? Ni hivi vilevile, imani peke yake pasipo matendo imekufa kabisa. Lakini mutu anaweza kusema: “Wewe uko na imani, na mimi niko na matendo.” Mimi nitajibu: “Unionyeshe imani yako pasipo matendo, na mimi nitakuonyesha imani yangu kwa njia ya matendo yangu.” Si wewe unaamini kwamba kuna Mungu mumoja? Ni vizuri! Hata pepo wanaamini vile, nao wanatetemeka kwa woga. Wewe mujinga! Unataka kuhakikishwa kwamba imani pasipo matendo ni bure? Babu yetu Abrahamu alihesabiwa haki mbele ya Mungu kwa njia ya matendo yake. Yeye alimutoa mwana wake Isaka juu ya mazabahu. Basi unaona kwamba imani yake ilionekana kwa njia ya matendo yake na kwa njia hiyo ikapata kukamilishwa. Na maandiko haya yakatimia: “Abrahamu alimwamini Mungu na kwa hiyo akahesabiwa kuwa mwenye haki.” Na Mungu akamwita rafiki yake. Basi munaona kwamba mutu anahesabiwa haki mbele ya Mungu kwa njia ya matendo, wala si kwa njia ya imani peke yake. Ilikuwa hivi vilevile kwa yule kahaba Rahaba. Mungu alimuhesabia haki kwa njia ya matendo yake, wakati alipowakaribisha wapelelezi na kuwatorosha kwa njia nyingine. Kwa maana kama vile mwili usiokuwa na pumzi ndani yake umekufa, hivi vilevile imani pasipo matendo imekufa. Wandugu zangu, kati yenu kusikuwe walimu wengi, kwa maana munajua vema ya kuwa sisi walimu tutahukumiwa vikali zaidi kuliko watu wengine. Sisi wote tunakosa kwa njia mbalimbali. Mutu asiyekosa katika masemi yake, huyo ni mutu mukamilifu, naye yuko na uwezo wa kutawala mwili wake wote. Tunaweka lijamu katika vinywa vya farasi kusudi watutii, na hivi tunaweza kuwaongoza kwenda fasi yote tunayotaka. Muangalie vilevile mashua. Hata mashua ni kubwa sana na zenye kusukumwa na upepo mukali, zinaongozwa na usukani mudogo sana na kuendeshwa pahali kapiteni anapotaka. Hivi vilevile ulimi ni kiungo kidogo cha mwili, lakini unaweza kujivunia mambo makubwa sana. Muangalie, moto kidogo inaweza kuchoma pori kubwa sana! Nao ulimi ni kama moto. Ulimi ni kiungo kinachojaa ubaya wa kila namna. Ulimi unapatikana kwenye nafasi yake katikati ya viungo vyetu, nao ndio unaochafua mwili wote. Unateketeza maisha yetu ukichomwa wenyewe na moto unaotoka katika jehenamu. Kila namna ya nyama, ndege, nyoka na samaki wanaweza kufugwa na mutu, na wamekwisha kufugwa naye. Lakini hakuna mutu mumoja anayeweza kufuga ulimi, maana ni uovu usiotulia, unajaa sumu yenye kuua. Kwa njia ya ulimi tunamusifu Bwana anayekuwa Baba yetu, na kwa njia ile ile tunalaani watu walioumbwa kwa mufano wa Mungu. Ndani ya kinywa kimoja munatoka maneno ya sifa na ya laana. Wandugu zangu, mambo haya hayapaswi kuwa vile. Maji matamu na maji machungu hayawezi kutiririka tokea fasi moja ndani ya kisima kimoja. Wandugu zangu, muti unaotoa matunda ya tini unaweza kutoa matunda ya muzeituni? Au muzabibu unaweza kutoa matunda ya tini? Hapana! Hivi vilevile kisima kinachotoa maji ya chumvi hakiwezi kutoa maji matamu. Nani anayekuwa na hekima na ufahamu kati yenu? Basi aonyeshe jambo lile kwa njia ya mwenendo wake muzuri, kwa njia ya matendo yanayofanyika katika upole unaotokana na hekima ile. Lakini mukiwa na wivu wenye kuchangana na uchungu katika mioyo yenu pamoja na roho ya ugomvi, musijivune wala musigeuze maneno ya kweli kuwa uongo. Hekima ya namna hii haitoki mbinguni; lakini ni ya dunia, nayo ni ya kimwili na ya kishetani. Kwa maana pahali kunapokuwa wivu na roho ya ugomvi, kuko machafuko vilevile na kila tendo baya. Lakini hekima inayotoka mbinguni, kwanza ni safi, tena ni yenye amani, upole na usikilivu, inajaa huruma na matendo mema. Haina upendeleo wala udanganyifu. Na tunda la haki linapandwa katika amani na wale wanaopenda amani. Magombano na ugomvi vinavyokuwa kati yenu vinatoka wapi? Si vinatoka katika tamaa zenu zinazopigana ndani ya miili yenu? Munatamani kupata kitu fulani, lakini hamukipati. Munaua na kusikia wivu, lakini hamuwezi kupata kitu. Na kwa hiyo, munagombana na kuwa na ugomvi. Hamupati kitu munachotaka kwa sababu hamukiombi kwa Mungu. Wakati munapoomba, hamupati kitu kwa sababu munaomba kwa nia mbaya, kwa maana munataka vitu kusudi mutimize tu tamaa zenu. Ninyi watu wasiokuwa na uaminifu! Hamujui kwamba kupenda raha ya dunia ni kuwa adui wa Mungu? Basi yeye anayetaka kupenda raha za dunia anajifanya mwenyewe kuwa adui wa Mungu. Musizani kwamba ni kwa bure Maandiko Matakatifu yanasema: “Mungu anasikia wivu sana kwa ajili ya yule Roho aliyemuweka akae ndani yetu.” Lakini Mungu ametujalia neema kubwa zaidi, kwa maana Maandiko yanasema: “Mungu anapingana na wenye kiburi, lakini anawajalia wanyenyekevu neema.” Basi mumutii Mungu. Mupingane na Shetani, naye atawakimbia. Mumukaribie Mungu, naye atawakaribia. Musafishe mikono yenu, ninyi wenye zambi! Mutakase mioyo yenu, ninyi wenye nia mbili! Musikitike, mulie na kulalamika. Kucheka kwenu kugeuke kuwa kilio, na furaha yenu igeuke kuwa huzuni. Mujinyenyekeze mbele ya Bwana, naye atawainua. Wandugu, musisemeane ubaya. Yule anayesema ubaya juu ya ndugu yake au kumuhukumu, anasema ubaya juu ya Sheria na kuihukumu. Ukihukumu Sheria, wewe si mwenye kutii Sheria, lakini mwenye kuihukumu. Mungu peke yake ndiye anayesimamisha Sheria na anayeweza kuhukumu. Ni yeye peke yake anayeweza kuokoa na kuangamiza. Basi wewe unayemuhukumu mwenzako, unajizania kuwa nani? Munisikilize sasa, ninyi munaosema: “Leo au kesho tutakwenda katika muji fulani, tutakaa kule kwa muda wa mwaka muzima, tutafanya biashara na kupata faida.” Ninyi hamujui namna gani maisha yenu yatakavyokuwa kesho! Kwa maana ninyi ni kama muvuke unaoonekana kwa wakati kidogo, kisha unatoweka. Ninyi mungepaswa kusema: “Kama Bwana anataka, tutaishi na kufanya hivi na hivi.” Lakini sasa munajivuna na kujisifu. Majivuno yote ya namna hii ni mabaya. Basi, mutu anayejua kutenda mema wala hayatendi, anafanya zambi. Basi, munisikilize sasa ninyi watajiri! Mulie na kuomboleza kwa sababu ya taabu itakayowapata. Mali yenu imeoza, na nguo zenu zimekuliwa na nondo. Zahabu na feza yenu vimepata kutu. Na kutu hii ndiyo itakayowashitaki, nayo itateketeza mwili wenu kama vile moto. Mumejiwekea akiba katika siku hizi za mwisho. Ninyi hamukulipa mishahara ya watumishi waliotumika katika mashamba yenu. Musikilize mashitaki yao! Malalamiko ya wavunaji yamefika katika masikio ya Bwana Mwenye Uwezo! Mumeishi katika utajiri na kujifurahisha katika maisha yenu katika dunia. Mumejinenepesha kwa kuwa tayari kwa siku ya kuchinjwa. Mumewahukumu na kuwaua wenye haki, nao hawakupingana nanyi. Basi wandugu, muvumilie mpaka Bwana atakaporudia. Muangalie namna mulimaji anavyongojea shamba litoe mavuno yanayokuwa ya faida kubwa. Yeye anavumilia mpaka wakati mvua ya kwanza na ya mwisho zinaponyesha. Nanyi vilevile, muvumilie na kutia mioyo yenu nguvu, kwa maana Bwana yuko karibu kurudi. Wandugu zangu, musinungunikiane ninyi kwa ninyi kusudi Mungu asiwahukumu. Muangalie, mwamuzi ni karibu, naye amekuwa kwenye mulango! Wandugu zangu, mukumbuke manabii waliotabiri kwa jina la Bwana, muangalie namna walivyovumilia katika mateso, nanyi mufuate mufano wao. Tunawaita watu hao kuwa wenye heri, kwa sababu walivumilia. Mumekwisha kusikia habari za uvumilivu wa Yobu, na munajua namna Bwana alivyomutendea kwa mwisho. Maana Bwana anajaa huruma na wema. Lakini zaidi ya yote, wandugu zangu, musiape! Musiape kwa jina la mbingu, wala kwa jina la dunia, wala kwa jina la kitu kingine chochote. Museme “Ndiyo” ikiwa munataka kusema ndiyo. Nanyi museme “Hapana” ikiwa munataka kusema hapana, kusudi musihukumiwe na Mungu. Kati yenu kuna mutu anayekuwa katika mateso? Aombe kwa Mungu. Au kuna mutu anayekuwa katika furaha? Aimbe nyimbo za sifa. Kati yenu kuna mugonjwa? Awaite wazee wa kanisa, nao watamwombea wakimupakaa mafuta kwa jina la Bwana. Nao wakiomba kwa imani, mugonjwa yule atapona, kwa kuwa Bwana atamurudishia afya yake. Na ikiwa amefanya zambi, atasamehewa. Basi muitikiane zambi ninyi kwa ninyi na kuombeana kusudi mupate kuponyeshwa. Maombi ya bidii ya mwenye haki ni yenye faida kubwa. Elia alikuwa mutu kama sisi. Yeye aliomba kwa bidii mvua isinyeshe, na mvua haikunyesha juu ya inchi kwa muda wa miaka mitatu na nusu. Kisha akaomba tena, na mbingu ikanyesha mvua, na inchi ikatoa mazao yake. Wandugu zangu, mutu mumoja kati yenu akipotea mbali na ukweli, na mutu mwingine akimurudisha, mukumbuke neno hili: yule anayemurudisha mwenye zambi toka njia ya upotevu ataokoa roho ya yule kutoka kifo, na zambi nyingi zitasamehewa. Barua hii inatoka kwangu mimi Petro, mutume wa Yesu Kristo. Ninawaandikia ninyi muliochaguliwa na Mungu na ambao mulisambazwa, na munaoishi kama wakimbizi kule Ponto, Galatia, Kapadokia, Azia na Bitinia. Mungu Baba aliwachagua ninyi tangu mbele kufuatana na mupango wake na kufanywa watakatifu na Roho, mupate kumutii Yesu Kristo na kusafishwa kwa damu yake. Ninawatakia neema na amani kwa uwingi. Tumusifu Mungu, Baba ya Bwana wetu Yesu Kristo! Kwa huruma yake kubwa ametupatia uzima mupya kwa njia ya kumufufua Yesu Kristo. Na kwa hiyo tumepata tumaini lenye uzima, na hivyo tutapata baraka zile ambazo Mungu aliwawekea watu wake. Baraka zisizoweza kuoza wala kuchafuka wala kupunguka; nazo zinawekewa akiba kwa ajili yenu mbinguni. Ninyi ambao kwa imani munalindwa salama kwa nguvu za Mungu kwa ajili ya wokovu ambao uko tayari kufunuliwa kwa mwisho wa nyakati. Katika mambo hayo yote mushangilie kwa furaha ijapokuwa inawapasa sasa kuhuzunika kwa wakati kidogo kwa ajili ya majaribu ya namna mbalimbali. Majaribu hayo ni kwa ajili ya kupima imani yenu. Zahabu ni kitu kinachoharibika, lakini ingawa vile inapimwa kwa njia ya kuchomwa ndani ya moto. Hivi vilevile imani yenu inayokuwa ya bei kali kuliko zahabu, inapaswa kupimwa kusudi ijulikane kuwa ya kweli. Na kwa sababu hii mutapata sifa, utukufu na heshima wakati Yesu Kristo atakapotokea. Ninyi munamupenda ijapokuwa hamujamwona, na munamwamini ijapokuwa sasa hamumwoni. Na zaidi ya ile munashangilia kwa furaha isiyoweza kuelezwa, inayojaa utukufu, kwa maana munapokea shabaha ya imani yenu, ni kusema wokovu wa roho zenu. Manabii walifanya uchunguzi na upelelezi juu ya wokovu ule, nao walitabiri juu ya zawadi ambayo ninyi mungepewa. Roho wa Kristo aliyekuwa ndani yao alitangulia kushuhudia mateso yatakayomupata Kristo na utukufu utakaokuwa nyuma. Nao walijitolea kusudi wapate kuvumbua wakati gani na kwa njia gani mambo haya yatafanyika. Mungu aliwafunulia wale manabii kwamba ujumbe ule walioutangaza haukuwaelekea wao wenyewe, lakini uliwaelekea ninyi. Na sasa ujumbe ule umetangazwa kwenu na wale waliowahubiri Habari Njema kwa uwezo wa Roho Mutakatifu aliyetumwa toka mbinguni. Hata wamalaika vilevile wanatamani kujua mambo hayo. Kwa sababu hiyo, mukuwe tayari kwa kutumikisha akili yenu. Mukeshe na muweke tumaini lenu lote katika baraka ile mutakayopewa wakati Yesu atakapotokea. Kama watoto wenye utii, musiachilie maisha yenu kutawaliwa na tamaa mbaya mulizokuwa nazo zamani wakati mulipokuwa mukiishi katika ujinga. Na sawa vile Mungu aliyewaita ni mutakatifu, ninyi vilevile munapaswa kuwa watakatifu katika mwenendo wenu wote. Kwa maana Maandiko Matakatifu yanasema: “Muwe watakatifu, kwa maana mimi ni mutakatifu.” Na ikiwa katika maombi yenu munamwita “Baba” yule anayehukumu kila mutu pasipo upendeleo kufuatana na matendo yake, basi muishi katika heshima mbele yake kwa muda unaowabakilia kwa kuishi hapa katika dunia. Kwa maana munajua namna gani mulivyokombolewa toka katika tabia za ovyo ovyo mulizoambukizwa na babu zenu. Hamukukombolewa kwa njia ya vitu vinavyoharibika kama vile feza au zahabu. Lakini mulikombolewa kwa njia ya damu yenye bei kali ya Kristo, aliyekuwa kama kondoo asiyekuwa na kilema wala uchafu. Yeye ndiye aliyechaguliwa na Mungu mbele ya kuumbwa kwa dunia, na alifunuliwa kwa ajili yenu katika nyakati hizi za mwisho. Kwa njia ya Kristo, ninyi munamwamini Mungu aliyemufufua na kumupa utukufu. Na kutokana na hiyo munamwamini Mungu na kumuwekea tumaini lenu. Ninyi mumekwisha kutakaswa kwa njia ya kutii neno la kweli kwa kuwapenda wandugu zenu pasipo unafiki. Basi mupendane kabisa, kwa moyo wenu wote. Kwa maana mumezaliwa upya, kwa nguvu za neno la Mungu lenye uzima na linalodumu hata milele. Nanyi si kama watoto waliozaliwa na wazazi wenye mwili huu unaokuwa wa kufa, lakini watoto waliozaliwa kwa nguvu ya uzazi usioweza kufa. Kwa maana Maandiko Matakatifu yanasema: “Wanadamu wote ni kama majani. Na utukufu wao wote unatoweka kama maua. Majani yanakauka na maua yanaanguka. Lakini Neno la Bwana linadumu hata milele.” Na Neno hili ni Habari Njema iliyohubiriwa kwenu. Basi, mutupilie mbali matendo yote maovu na ya udanganyifu pamoja na wivu na masingizio ya kila namna. Kama vile watoto wachanga wanaotamani maziwa, na ninyi vilevile mukuwe na hamu ya kunywa maziwa safi ya kiroho, kusudi mupate kukomaa na kuokolewa. Kwa maana Maandiko Matakatifu yanasema: “Mumetambua kwamba Bwana ni mwema.” Mumwendee Bwana. Yeye ni jiwe lenye uzima. Jiwe lile lilitupiliwa na watu lakini lilichaguliwa na Mungu, nalo linahesabiwa kuwa la bei kali mbele yake. Nanyi vilevile, kama mawe yenye uzima mutumiwe kwa kujenga hekalu la kiroho. Na mule mutafanya kazi takatifu ya ukuhani kwa kutoa sadaka za kiroho zinazomupendeza Mungu kwa njia ya Yesu Kristo. Kwa kuwa imeandikwa hivi katika Maandiko Matakatifu: “Nimesimika jiwe kubwa la pembe katika Sayuni, jiwe lile ni la bei kali. Ni mimi niliyelichagua. Yule anayelitumainia hatapata haya.” Basi jiwe lile linahesabiwa kuwa la bei kali kwa wale wanaoamini. Lakini kwa wale wasioamini ni: “Jiwe lililotupiliwa na wajengaji, lakini sasa linakuwa jiwe kubwa la pembe.” Tena imeandikwa kwamba: “Jiwe lile ni la kukwalisha watu, nalo ni la kuwaangusha.” Wamejikwaa kwa sababu hawakuamini neno la Mungu, na hivi ndivyo walivyopanga kwa ajili yao tangu mwanzo. Lakini ninyi ni watu wa kizazi kilichochaguliwa na Mungu na wa ukuhani wa kifalme. Ninyi ni taifa takatifu na watu wa pekee wa Mungu. Mumechaguliwa kusudi mutangaze matendo makubwa ya yule aliyewaita kutoka katika giza na kuwaingiza kwenye mwangaza wake wa ajabu. Zamani ninyi hamukukuwa watu wa Mungu, lakini sasa munakuwa watu wake; zamani ninyi hamukuhurumiwa na Mungu, lakini sasa mumehurumiwa naye. Wapendwa wangu, ninawasihi ninyi, kama vile wageni na wasafiri hapa katika dunia, muepuke tamaa za mwili zinazopigana na roho. Mukuwe na mwenendo muzuri kati ya wapagani, kusudi wakiwasingizia kwamba mumefanya mabaya, wapate kuona matendo yenu mema na wamutukuze Mungu siku ile ya kuja kwake. Kwa ajili ya utukufu wa Bwana, mutii mamlaka yote ya watu: ikiwa ni mufalme anayekuwa na uwezo juu ya vyote, au ikiwa maliwali waliosimikwa naye kwa kuwaazibu watenda mabaya na kuwapa zawadi wale wanaotenda mema. Na hayo ndiyo mapenzi ya Mungu, anayetaka munyamazishe usemi wa ujinga wa wapumbafu kwa njia ya kutenda mema. Muishi kama watu wanaokuwa na uhuru, lakini musitumie uhuru wenu kwa kufunika ubaya, lakini muishi kama watumwa wa Mungu. Muwaheshimu watu wote. Muwapende wandugu zenu waamini. Mumwogope Mungu, mumuheshimu mufalme. Ninyi watumishi, muwatii wabwana wenu na kuwapa heshima yote, si wale wanaokuwa wema na wapole tu, lakini hata wale wanaokuwa wakali vilevile. Kwa maana mukivumilia mateso musiyostahili kwa ajili ya kumuheshimu Mungu, yeye atawabariki. Kuna sifa gani kama mukivumilia mapigo kwa sababu mulitenda mabaya? Lakini mukivumilia mateso kwa sababu mulitenda mema, jambo hilo linamupendeza Mungu. Ni kwa ajili ya shabaha hiyo Mungu aliwaita kumufuata, kwa sababu Kristo vilevile aliteswa kwa ajili yenu, akiwaachia mufano, kusudi mufuate njia yake. Yeye hakutenda zambi, wala neno la udanganyifu halikutoka ndani ya kinywa chake. Wakati walipomutukana, hakurudisha matukano; alipoteswa, hakutisha watu hata wamwogope. Lakini alijiachilia katika mikono ya Mungu anayehukumu watu kwa haki. Kristo yeye mwenyewe alibeba mizigo ya zambi zetu ndani ya mwili wake alipoteswa juu ya musalaba, kusudi tupate kuachana na zambi kabisa na kuishi maisha ya haki. Kwa ajili ya mapigo yake ninyi muliponyeshwa. Kwa maana mulikuwa kama kondoo wanaopotea, lakini sasa mumerudi kwa yule anayekuwa muchungaji na mwangalizi wa roho zenu. Ninyi wake, muwatii waume wenu, kusudi kukiwa wamoja kati yao wasioamini neno la Mungu, mupate kuwavuta kwa kulisadiki kwa mwenendo wenu muzuri pasipo kuwaambia neno. Wataweza kuvutwa kwa kuona mwenendo wenu safi na wa heshima. Kujipamba kwenu kusikuwe kwa inje sawa vile kusuka nywele, kuvaa mapambo ya zahabu au nguo za bei kali. Lakini mapambo yenu yanapaswa kuwa ya ndani ya moyo yasiyoweza kuharibika. Sherti mapambo yale yakuwe yenye kutokana na roho ya amani na upole inayohesabiwa kuwa ya bei kali mbele ya Mungu. Kwa maana ni vile ndivyo wanawake waliomwabudu Mungu kwa kweli na kumutumainia walivyojipamba wakiishi katika utii mbele ya waume wao. Ni vile Sara alimutii Abrahamu, akimwita “Bwana.” Ninyi ni wabinti zake kama mukifanya mema pasipo kuogopa kitisho chochote. Vilevile, ninyi waume, mukae na wake wenu mukifahamu kwamba wao ni kiumbe kizaifu. Munapaswa vilevile kuwapa heshima kwa sababu watapokea pamoja nanyi zawadi ya uzima. Mufanye hivi kusudi maombi yenu yasizuizwe. Kwa kumaliza, ninyi wote mukuwe na mawazo na nia moja, mupendane kama wandugu waamini, mukuwe wema na wanyenyekevu. Musirudishiane mabaya kwa mabaya au matusi kwa matusi, lakini muombeane baraka, kwa sababu Mungu aliahidi kuwabariki ninyi wakati alipowaita kumufuata. Kwa maana Maandiko Matakatifu yanasema: “Kuna mutu anayependa kuishi vizuri, na kukaa katika siku za heri? Azuize ulimi wake na mabaya nayo midomo yake na uongo. Aepuke mabaya, atende mema, atafute amani na kuifuatilia. Kwa maana macho ya Bwana yanawaelekea wenye haki, nayo masikio yake yanasikiliza maombi yao. Lakini uso wa Bwana unawapinga waovu.” Ni nani atakayewazuru ninyi kama mukiwa wenye bidii katika kutenda mema? Hata mukiteswa kwa ajili ya haki, ninyi ni wenye heri. Musiwaogope watu, wala musihangaike. Lakini mumutukuze Bwana wenu Kristo ndani ya mioyo yenu. Mukuwe tayari wakati wowote kumujibu kila mutu anayewauliza juu ya tumaini munalokuwa nalo. Lakini mufanye vile kwa upole na heshima, mukiwa na zamiri safi, hata wale wanaowasingizia na kuwatukana juu ya mwenendo wenu muzuri katika ushirika wenu na Kristo, wapate haya. Kwa maana kuteswa kwa ajili ya kutenda mema, ikiwa ni mapenzi ya Mungu, ni vizuri kuliko kuteswa kwa ajili ya kutenda mabaya. Kufuatana na hiyo, Kristo naye alikufa mara moja tu kwa sababu ya zambi zenu. Yeye alikuwa mwenye haki kwa ajili ya waovu, kusudi awaonyeshe ninyi njia ya kumufuata Mungu. Aliuawa kimwili, lakini kwa uwezo wa Roho Mutakatifu alipata tena uzima. Kwa njia ya huyu Roho alienda hata kuhubiri roho zilizokuwa katika kifungo. Roho zile ni za watu walioasi Mungu zamani za kale alipowavumilia katika siku Noa alipotengeneza chombo kikubwa. Ni watu wanane tu ndio waliingia ndani ya chombo na kuokolewa katika maji. Maji haya ni mufano wa ubatizo unaowaokoa ninyi sasa. Ubatizo ule si kwa ajili ya kusafisha uchafu wa mwili lakini ni njia ya kufanya mapatano na Mungu katika zamiri safi. Nao unawaokoa ninyi kwa njia ya ufufuko wa Yesu Kristo, aliyepanda mbinguni, na anayekaa na mamlaka kwa kuume kwa Mungu, akitawala wamalaika, nao wenye mamlaka na uwezo wanaokuwa katika mbingu. Kristo aliteswa kimwili. Basi ninyi vilevile mujikaze mupate kuwa na nia kama ile yake. Kwa maana mutu anayevumilia mateso ya mwili, anaachana kabisa na zambi. Sasa, musiishi tena kufuatana na tamaa za kimutu, lakini muishi kufuatana na mapenzi ya Mungu kwa muda unaowabakilia kwa kukaa katika dunia. Kufuatana na hiyo, zamani mulipitisha siku nyingi mukifanya matendo yanayolingana na ya wapagani. Mulizoea kuishi katika uasherati, tamaa mbaya, ulevi, karamu za ulafi, za ulevi na kuabudu sanamu. Sasa, wapagani wanashangaa kuona ninyi hamushirikiani nao tena katika maisha ya ovyo ovyo; na kwa hiyo wanawasingizia ninyi. Lakini watu hawa watasamba maneno yao mbele ya Mungu anayekwisha kuwa tayari kwa kuhukumu wafu na wazima. Kwa sababu hiyo Habari Njema ilitangazwa kwa wafu, kwa wale waliohukumiwa kimwili sawa watu wengine, kusudi wapate kuishi kiroho kama vile Mungu anavyoishi. Mwisho wa vitu vyote unakaribia kutimia. Kwa hiyo mukuwe wenye akili na waangalifu, kusudi mukuwe na uwezo wa kuomba. Na zaidi ya yote mudumu katika upendo ninyi kwa ninyi, maana upendo unafunika zambi nyingi. Mukaribishane ninyi kwa ninyi pasipo kunungunika. Kila mutu kati yenu anapaswa kuitumia zawadi ya kiroho aliyojaliwa na Mungu kwa ajili ya mafaa ya wengine. Na hivi mutakuwa walinzi wazuri wa zawadi mbalimbali mulizopewa na Mungu. Yule anayehubiri, anapaswa kutoa ujumbe wa Mungu. Na yule anayetumika, atumike kwa kadiri ya nguvu alizopewa na Mungu, kusudi Mungu atukuzwe katika mambo yote kwa njia ya Yesu Kristo anayekuwa mwenye utukufu na uwezo kwa milele na milele. Amina. Wandugu wapendwa, musishangae kwa kuona mateso makubwa ya kuwajaribu munayopata. Musiyahesabu kuwa kitu kigeni kwenu. Lakini mufurahi kwa sababu munashiriki katika mateso ya Kristo. Na kwa hiyo mutashangilia kwa furaha wakati atakapoonekana katika utukufu. Ninyi ni wenye heri kama watu wakiwatukana kwa ajili ya Kristo, kwa kuwa Roho wa utukufu, maana yake Roho wa Mungu anakaa ndani yenu. Kati yenu kusikuwe hata mutu mumoja anayeteswa kwa sababu yeye ni mwuaji, mwizi, mutenda mabaya au mwenye kujiingiza katika mambo ya watu wengine. Lakini mutu akiteswa kwa sababu yeye ni mukristo, asione haya, lakini atukuze Mungu kwa kuwa anaitwa kwa jina lile. Wakati wa hukumu unakaribia. Na hukumu itaanza na watu wa Mungu. Na kama hukumu inaanzia kwetu sisi, basi mwisho wake utakuwa namna gani kwa wale wasiotii Habari Njema ya Mungu? Ni kama vile Maandiko haya Matakatifu yanavyosema: “Ikiwa hata kuokolewa kwa mwenye haki ni kugumu; itakuwa namna gani kwa mwovu na mwenye zambi?” Basi watu wanaoteswa kwa ajili ya kufanya mapenzi ya Mungu, waendelee kutenda mema, nao watoe roho yao katika mikono ya Mungu Muumba wao anayekuwa mwaminifu kabisa. Ninawaonya wazee wa kanisa wanaokuwa kati yenu. Mimi vilevile ni muzee mwenzenu, nami ni mushuhuda wa mateso ya Kristo na zaidi ya hii nitashiriki katika utukufu ule utakaotokea. Ninawaonya, muchunge lile kundi Mungu alilowapatia, si kwa kulazimishwa, lakini kwa mapenzi yenu sawa vile Mungu anavyotaka. Musitumike kwa ajili ya tamaa mbaya ya mali, lakini kwa kujitoa kwa moyo mwema. Musitawale kwa kinguvu kundi lile lililowekwa chini ya uangalizi wenu, lakini mukuwe mifano kwao. Na wakati Muchungaji Mukubwa atakapotokea, mutapokea taji ya utukufu isiyoweza kuharibika. Na hivi vilevile, ninyi vijana, munapaswa kuwatii hao wazee. Ninyi wote munapaswa kuwa na unyenyekevu, mupate kutumikiana; maana Maandiko Matakatifu yanasema: “Mungu anawapinga wenye kiburi, lakini anawajalia wanyenyekevu neema.” Basi mujinyenyekeze mbele ya Mungu mwenye uwezo, kusudi awainue kwa wakati unaofaa. Mumutolee masumbuko yenu yote kwa maana yeye anawashugulikia. Mukuwe waangalifu na mukeshe, kwa maana adui yenu Shetani anazungukazunguka kama simba anayenguruma akitafuta yule atakayerarua. Mupingane naye, mukisimama imara katika imani, mukijua kwamba fasi zote katika dunia, wandugu zenu wanapata mateso kama hayo. Lakini mukisha kuteswa kwa muda kidogo, Mungu mwenye neema yote aliyewaita kusudi mupate kushiriki naye katika utukufu wake wa milele katika kuungana kwenu na Kristo, yeye mwenyewe atawakamilisha. Atawatia nguvu na kuwasimamisha imara kabisa. Yeye ndiye Mungu mwenye uwezo kwa milele na milele. Amina. Nimewaandikia barua hii fupi nikisaidiwa na Sila, ninayemujua kuwa ndugu mwaminifu. Ninataka kuwatia moyo na kushuhudia kwenu kwamba mambo hayo yanayoelekea neema ya Mungu ni ya kweli; nanyi musikose kushikamana nayo. Kanisa linalokuwa katika Babeli, lililochaguliwa na Mungu kama vile ninyi, linawasalimia. Vilevile Marko, mwana wangu katika imani, anawasalimia. Musalimiane kwa upendo wa kindugu. Ninawatakia amani ninyi watu wote wa Kristo. Barua hii inatoka kwangu mimi Simoni Petro, mutumishi na mutume wa Yesu Kristo. Ninawaandikia ninyi mulioshiriki pamoja nasi katika imani ile inayokuwa kubwa kwa njia ya haki ya Mungu wetu na Mwokozi Yesu Kristo. Ninawatakia neema na amani kwa uwingi kufuatana na vile munavyomujua Mungu na Yesu Bwana wetu. Kwa uwezo wake, Mungu ametujalia mambo yote tunayohitaji katika maisha yetu kusudi tupate kushikamana na kumwabudu yule aliyetuita kushiriki utukufu wa wema wake mwenyewe. Kufuatana na hayo, ametupatia ahadi nzuri sana na kubwa mupate kuepuka uharibifu unaoletwa na tamaa mbaya za dunia na kushika hali yake ya kimungu. Na kwa sababu hii, mufanye bidii ya kuongeza wema juu ya imani yenu, elimu juu ya wema wenu, ukadirifu juu ya elimu yenu, uvumilivu juu ya ukadirifu, kushikamana na ibada juu ya uvumilivu, undugu juu ya kushikamana na ibada, na upendo juu ya undugu wenu. Kwa maana mukiwa na tabia hizi zote kwa uwingi, zitawawezesha kutumika na kuzaa matunda hata mupate kumujua Bwana wetu Yesu Kristo. Lakini mutu asiyekuwa na tabia hizo ni kipofu, hawezi kuona. Yeye amesahau kwamba amekwisha kutakaswa zambi zake za zamani. Kwa hiyo wandugu zangu, kufuatana na vile mulivyochaguliwa na kuitwa na Mungu, mufanye nguvu zaidi kwa kukamilika katika njia ile. Mukitenda mambo yale hamutaanguka hata kidogo. Maana kwa kufanya vile, mutaruhusiwa kabisa kuingia katika Ufalme wa milele wa Bwana na Mwokozi wetu Yesu Kristo. Kwa sababu hii, nitaendelea kuwakumbusha mambo haya siku zote ingawa mumekwisha kuyafahamu na kukamilika katika ukweli muliopokea. Ninaona kwamba ni vema niwaamushe kwa njia ya kuwakumbusha mambo haya wakati wote wa maisha yangu. Kwa maana ninajua kwamba ninakaribia kuacha mwili huu unaokuwa wa kufa kama vile Bwana wetu Yesu Kristo alivyonionyesha waziwazi. Nitajikaza sana kuwapatia njia ya kuweza kukumbuka mambo haya siku zote kisha kufa kwangu. Basi, wakati tulipowajulisha uwezo na kurudia kwa Bwana wetu Yesu Kristo, sisi hatukutumia hadisi za uongo zilizotungwa kwa werevu. Lakini tulijionea na macho yetu sisi wenyewe uwezo wake. Maana alipokea heshima na utukufu toka kwa Mungu Baba, wakati sauti yenye utukufu mukubwa toka kwa Mungu ilipomufikia ikisema: “Huyu ni Mwana wangu mupendwa, ninapendezwa naye sana!” Sisi wenyewe tuliisikia sauti ile toka mbinguni tulipokuwa pamoja naye juu ya mulima mutakatifu. Vilevile tunaamini ujumbe uliotangazwa na manabii. Ninyi munafanya vema mukishikamana nao. Ujumbe huo ni kama taa inayoangaza pahali pa giza, mpaka wakati wa mapambazuko na wakati nyota ya asubui itakapoangazia mioyo yenu. Mbele ya yote, mujue kwamba hakuna mutu anayeweza kufasiria yeye mwenyewe unabii unaokuwa katika Maandiko Matakatifu. Maana hakuna hata ujumbe wowote uliotetewa kwa mapenzi ya kimutu, lakini watu walipasha ujumbe wa Mungu wakiongozwa na Roho Mutakatifu. Zamani manabii wa uongo walitokea kati ya watu, na ndivyo hivyo walimu wa uongo watakavyotokea kati yenu. Watu hawa wataingiza mafundisho mabaya sana ya uongo kwa siri, wakimukataa hata Bwana aliyewakomboa na kujiletea maangamizi upesi. Watu wengi watafuata matendo yao maovu na kwa ajili yao, mafundisho ya Bwana yatazarauliwa. Na kwa sababu ya tamaa yao mbaya ya mali, walimu hawa wa uongo watajipatia faida juu yenu kwa njia ya maneno ya uongo. Lakini tangia zamani hukumu yao imekwisha kutangazwa, nao hawatakawia kuangamizwa. Kwa maana Mungu hakuwahurumia wale wamalaika waliofanya zambi, lakini aliwatupa katika jehenamu. Wao wanalindwa mule wakifungwa minyororo katika giza nzito wakingojea Siku ile ya hukumu. Mungu hakuhurumia dunia ya zamani, lakini alimulinda Noa, muhubiri wa haki, pamoja na watu wengine saba alipoleta mafuriko ya maji juu ya dunia ile ya waovu. Vilevile Mungu alihukumu muji wa Sodoma na Gomora na kuiteketeza kwa moto. Kwa njia hiyo, alionyesha mufano wa mambo yatakayotokea kwa watu waovu. Mungu alimwokoa Loti, mutu wa haki, aliyehuzunishwa sana na mwenendo mubaya wa wale watu waovu. Kwa maana mutu yule mwenye haki aliishi kati ya watu wabaya, akiona na kusikia kila siku mambo yaliyochukiza roho yake ya haki. Basi, ni kusema kwamba Bwana anajua namna ya kuwaokoa wenye kumwogopa katika majaribu. Lakini anangojea kuwaazibu watu wabaya kwa Siku ile ya hukumu. Na zaidi atawaazibu wale wanaoishi kufuatana na tamaa mbaya za kimwili na kuzarau mamlaka ya Mungu. Walimu wale wa uongo ni wenye kiburi, wenye kujivuna, nao hawaogopi kutukana viumbe vitukufu vya mbinguni. Ingawa vile, wamalaika wenye kuwapita nguvu na uwezo hawawashitaki vibaya kwa kuwatukana mbele ya Bwana. Walimu hawa wa uongo ni kama nyama wasiokuwa na akili ambao wanazaliwa tu kwa kunaswa na kuchinjwa. Wao wanasema vibaya juu ya mambo yote wasiyojua. Wataangamizwa kufuatana na ubaya wao wenyewe. Watalipwa mateso kwa sababu ya mateso waliyoleta. Wanafurahia kutimiza waziwazi tamaa zao mbaya za kimwili muchana kati. Kufika kwao katika karamu zenu kunaleta haya na chukizo kubwa wanapofurahia mambo yao ya udanganyifu. Macho yao yanajaa uzinzi. Wao hawachoki kufanya zambi. Wanavuta watu wasiokamilika. Wanatawaliwa na tamaa za kupata mali. Watu hao wamelaaniwa! Wameacha njia ya kweli na kupotoka wakifuata njia ile Balama, mwana wa Beori, aliyofuata. Huyu alipenda kupata mali kwa njia isiyokuwa ya haki, lakini alikaripiwa kwa ajili ya uovu wake. Basi punda, ambaye hasemi, alisema kama mutu na kuzuiza kitendo cha upumbafu wa yule nabii. Wale walimu wa uongo ni kama visima visivyokuwa na maji tena, wao ni kama mawingu yanayopeperushwa na upepo; makao yao yametayarishwa kwenye giza nzito. Kwa maana kwa masemi yao ya kujivuna na yasiyokuwa na maana, na kwa njia ya tamaa zao mbaya za kimwili, wanawavuta watu ambao wanaanza kuwaepuka, na wale wanaoishi katika udanganyifu. Wanawaahidi watu wengine kwamba watakuwa huru ijapokuwa wao wenyewe ni watumwa wa upotovu. Kwa maana kila mutu ni mutumwa wa jambo lolote linalomutawala. Kufuatana na hayo, ikiwa watu wamekwisha kuponyoka kuishi katika machafuko ya dunia kwa njia ya kumujua Bwana na Mwokozi wetu Yesu Kristo, nao wakiyarudilia tena na kutawaliwa nayo, hali yao ya mwisho itakuwa mbaya zaidi kuliko ile ya kwanza! Maana ingekuwa heri kwao kama wasingejua njia ya haki, kuliko kuijua na kisha kuacha ile amri takatifu waliyopewa. Kile kitu walichofanya kinaonyesha wazi mufano unaosema: “Imbwa amerudilia kula matapiko yake,” na: “Nguruwe aliyesafishwa amerudia tena kugaagaa katika matope!” Wapendwa wangu, hii ni sasa barua ya pili ninawaandikia. Katika barua hizi zote mbili nilitaka kuamusha ndani yenu mafikiri safi mupate kukumbuka mambo haya. Ninataka mukumbuke maneno yaliyosemwa zamani na manabii watakatifu na ile amri ya Bwana na Mwokozi muliyotolewa na mitume wenu. Mbele ya yote, mujue kwamba katika siku za mwisho kutakuja watu watakaoishi kufuatana na tamaa zao wenyewe. Watawachekelea ninyi na kusema: “Aliahidi kwamba atakuja! Sasa yeye yuko wapi? Kwa maana, tangia kufa kwa babu zetu mambo yote yanaendelea kubakia sawa vile yalivyokuwa tangu kuumbwa kwa dunia.” Watu hawa wanasahau kwa makusudi kwamba tangia zamani Mungu alisema tu, na mbingu na dunia vikakuwa. Dunia iliumbwa toka katika maji na kwa njia ya maji. Vilevile kufuatana na ile, dunia ya zamani iliangamizwa kwa mafuriko ya maji. Lakini kwa nguvu ya neno lile lile, mbingu na dunia za sasa zimewekwa akiba kwa kuteketezwa kwa moto. Zinalindwa kwa ajili ya Siku ile ambayo watu wabaya watahukumiwa na kuangamizwa. Lakini wapendwa wangu, kuna jambo moja musilopaswa kusahau: ni kwamba mbele ya Bwana, siku moja ni kama miaka elfu moja na miaka elfu moja ni kama siku moja. Bwana hakawii kutimiza ahadi zake kama vile watu wamoja wanavyozania. Yeye anavumilia kwa ajili yenu, maana hapendi hata mutu mumoja apotee, lakini anataka watu wote wageuke toka zambi zao. Siku Bwana atakaporudi, itatimia kama vile mwizi anavyokuja. Siku ile mbingu zitatoweka kwa shindo kubwa, na viumbe vyote vinavyoangaza katika mbingu vitayeyuka. Dunia na vitu vyote vinavyokuwa ndani yake vitateketezwa. Basi kwa kuwa vitu vyote vitaharibiwa namna hii, ninyi munapaswa kuishi maisha matakatifu na kushikamana na ibada, mukingojea na kuharikisha kuja kwa Siku ile ya Mungu; ndiyo siku mbingu zitakapoyeyushwa kwa moto, na viumbe vyote vinavyoangaza katika mbingu vitakapoyeyuka. Lakini, kufuatana na ahadi ya Mungu, tunangojea kwamba kutakuwa mbingu mupya na dunia mupya, pahali haki itakapokuwa. Kwa sababu hiyo, wapendwa wangu, mukiwa munangojea mambo yale, mufanye bidii apate kuwakuta safi bila kosa lolote na mukae na amani pamoja naye. Mutambue kwamba njia ya kuvumilia kwa Bwana wetu ni wakati muzuri anaowapatia kusudi mupate kuokolewa. Na hiyo ni kufuatana na vile ndugu yetu mupendwa Paulo alivyowaandikia akiongozwa na hekima aliyopewa na Mungu. Ni vile ndivyo alivyoandika katika barua zote alimosema ndani yao juu ya mambo yale. Lakini ndani ya barua zile kunakuwa mambo mengine magumu kuyasikia. Na watu wajinga na wasiokamilika wanageuzageuza maana yake sawa vile wanavyogeuza sehemu zingine za Maandiko Matakatifu. Kwa njia ile wanajiangamiza wenyewe. Basi ninyi wapendwa wangu, mumekwisha kutambua mambo haya. Mujiangalie vizuri kusudi musipotoshwe na makosa ya watu waovu na kukosa kusimama imara. Lakini muzidi kukomaa katika neema na katika kumujua Bwana na Mwokozi wetu Yesu Kristo. Asifiwe, sasa na hata milele! Amina. Tunawaandikia ninyi juu ya Neno la uzima, lililokuwa tangia mwanzo. Sisi tulilisikia, tuliliona kwa macho yetu wenyewe, tuliliangalia na kuligusa kwa mikono yetu wenyewe. Uzima huu ulipotokea, sisi tuliuona. Kwa sababu hii tunaushuhudia na kuwatangazia habari za huo uzima wa milele, uliokuwa pamoja na Baba na ulioonyeshwa kwetu. Lile tuliloona na kulisikia, ndilo tunalotangaza kwenu vilevile, kusudi mupate kushirikiana nasi. Na huu ushirika wetu ni ule tunaokuwa nao pamoja na Baba na Mwana wake Yesu Kristo. Tunawaandikia ninyi maneno haya kusudi tupate kujazwa na furaha kabisa. Na hii ndiyo habari tuliyoisikia kutoka kwa Yesu Kristo na kuitangaza kwenu: Mungu ni mwangaza, na ndani yake hamuna giza hata kidogo. Tukisema kwamba tunashirikiana naye, lakini tunaishi katika giza, tunasema uongo, nayo matendo yetu si ya kweli. Lakini kama tunaishi katika mwangaza kama vile Mungu mwenyewe anavyokaa katika mwangaza, tunashirikiana sisi kwa sisi, na damu ya Mwana wake Yesu inasafisha zambi zetu zote. Tukisema kwamba hatuna zambi, tunajidanganya sisi wenyewe, wala ukweli hauko ndani yetu. Lakini tukiitikia zambi zetu mbele ya Mungu, yeye atatusamehe zambi zetu na kutusafisha toka katika maovu yote kwa maana yeye ni mwaminifu na mwenye haki. Tukisema kwamba hatukutenda zambi, tunamugeuza Mungu kuwa mwongo, na ukweli wa neno lake si ndani yetu. Watoto wangu wapendwa, ninawaandikia maneno hayo kusudi musitende zambi. Lakini kama mutu akitenda zambi, tuko na yule anayetutetea mbele ya Baba. Naye muteteaji yule ndiye Yesu Kristo, mwenye haki. Yeye ndiye sadaka iliyotolewa kwa ajili ya usamehe wa zambi zetu, wala si kwa ajili ya zambi zetu tu, lakini kwa ajili ya zambi za watu wote. Sisi tunatambua kwamba tunamujua Mungu ikiwa tunashika amri zake. Mutu akijidai kwamba anamujua Mungu, lakini hashiki amri zake, yeye ni mwongo, nao ukweli hauko ndani yake. Lakini yule anayetii neno la Mungu yuko na upendo kamili wa Mungu ndani yake. Hili ndilo jambo linalotuonyesha kwamba sisi tunaungana na Mungu: mutu yeyote anayesema kwamba anaungana na Mungu anapaswa kuishi sawa vile Yesu alivyoishi. Wapenzi, siwaandikii amri mupya, lakini ile ya zamani muliyoijua tangia mbele. Na amri hiyo ya zamani ni lile neno mulilosikia. Kwa ngambo ingine amri hii ninayowaandikia ni mupya, na ukweli wake unaonekana ndani ya Kristo na ndani yenu vilevile. Kwa maana giza linapita na mwangaza wa kweli umekwisha kutokea. Mutu anayesema kwamba anaishi katika mwangaza, lakini anamuchukia ndugu yake, yeye angali anaishi katika giza. Yule anayemupenda ndugu yake, anaishi katika mwangaza na ndani yake hamuna kitu kinachoweza kuangusha mwingine katika zambi. Lakini anayemuchukia ndugu yake anaishi na kutembea katika giza, wala hajui pahali anapokwenda kwa sababu giza limemupofusha macho. Ninawaandikia ninyi watoto wangu, kwa sababu mumesamehewa zambi zenu kwa jina la Kristo. Ninawaandikia ninyi wababa, kwa sababu mumemujua yule aliyekuwa tangu mwanzo wa vitu vyote. Ninawaandikia ninyi vijana kwa sababu mumemushinda yule Mwovu. Nimewaandikia ninyi watoto, kwa sababu mumemujua Baba. Ninawaandikia ninyi wababa, kwa sababu mumemujua yule aliyekuwa tangia mwanzo wa vitu vyote. Ninawaandikia ninyi vijana, kwa sababu muko na nguvu na Neno la Mungu linakaa ndani yenu, nanyi mumemushinda yule Mwovu. Musipende dunia, wala mambo yanayokuwa katika dunia. Mutu akipenda dunia, hawezi kumupenda Mungu Baba. Kwa maana kila kitu kinachokuwa katika dunia, kama vile tamaa ya kimwili, tamaa ya macho, na majivuno ya maisha, hivi vyote havitoki kwa Baba, lakini vinatoka katika dunia. Dunia inapita pamoja na tamaa zake, lakini mutu yule anayefanya mapenzi ya Mungu anaishi milele. Watoto wangu, huu ni wakati wa mwisho. Mulisikia habari kwamba mupinga Kristo atakuja, lakini hata sasa wapinga Kristo wengi wametokea. Na kwa hiyo tunajua kwamba ni wakati wa mwisho. Watu hawa wametoka kati yetu, lakini hawakukuwa wa kundi letu, na kwa sababu hii wametuacha. Kama wangekuwa wa kundi letu, wangekaa pamoja nasi. Lakini wametuacha kusudi ionekane wazi ya kama hawakukuwa wa kundi letu. Lakini munajazwa na Roho Mutakatifu ambaye Kristo alimimia juu yenu, na kwa hiyo ninyi wote munajua ukweli. Basi, sikuwaandikia kwa sababu hamujui ukweli, lakini kwa sababu munaujua na tena kwa sababu hakuna uongo wowote unaoweza kutokana na ukweli. Ni nani anayekuwa musema uongo? Ni yule anayekana kwamba Yesu si Kristo. Huyu ndiye mupinga Kristo, kwa maana anamukana Baba na Mwana. Yule anayemukana Mwana, anamukana Baba vilevile, lakini yule anayemukubali Mwana, anamukubali Baba vilevile. Kwa hiyo muchunge ndani ya mioyo yenu mafundisho muliyosikia tangia mbele. Kama mukichunga mafundisho yale muliyosikia tangia mbele, mutakaa ndani ya Mwana pamoja na Baba. Na Kristo yeye mwenyewe alituahidi sisi uzima wa milele. Nimewaandikia maneno hayo kwa sababu ya watu wanaotafuta kuwadanganya. Lakini Kristo amemimia Roho juu yenu. Na kufuatana na vile Roho yule anavyokaa ndani yenu, hamuhitaji kufundishwa na mutu, kwa maana Roho wake anawafundisha mambo yote. Roho yule anasema ukweli wala hasemi uongo. Basi kama vile Roho alivyowafundisha, mukae ndani ya Kristo. Na sasa watoto wangu, mukae ndani yake kusudi tukuwe na tumaini hakika wakati atakapotokea, na kutosikia haya mbele yake siku atakaporudi. Munajua kwamba Kristo ni mwenye haki, kwa hiyo munapaswa kujua vilevile kwamba kila mutu anayefuata haki ni mutoto wa Mungu. Muangalie namna Baba alivyoonyesha upendo wake kwetu hata tupate kuitwa watoto wa Mungu! Na kwa hakika sisi ndio wao! Ndiyo maana watu wa dunia hawatutambui, kwa sababu hawakumujua Mungu. Wapendwa wangu, sasa sisi ni watoto wa Mungu, wala namna tutakavyokuwa haijaonekana bado waziwazi. Lakini tunajua kwamba wakati Kristo atakapotokea, tutafanana naye kwa sababu tutamwona vile anavyokuwa. Basi, kila mutu anayekuwa na tumaini hili katika Kristo anajisafisha mwenyewe kama vile Kristo anavyokuwa safi. Kila mutu anayefanya zambi anavunja sheria ya Mungu, kwa sababu kufanya zambi ni kuvunja sheria. Ninyi munajua kwamba Yesu Kristo alikuja kusudi aondoe zambi, na hakuna zambi ndani yake. Basi kila mutu anayeungana naye hafanyi tena zambi; lakini kila mutu anayefanya zambi hakumwona wala kumujua. Watoto wangu, mutu asiwadanganye! Mutu anayetenda mambo ya haki ni mwenye haki kama vile Kristo ni mwenye haki. Mutu anayefanya zambi ni mutu wa Shetani, kwa maana Shetani anafanya zambi tangia mwanzo wa vitu vyote. Kwa sababu hii, Mwana wa Mungu alikuja kusudi aharibu kazi za Shetani. Kila mutu anayekuwa mutoto wa Mungu hafanyi zambi, kwa sababu neno la Mungu linakaa ndani yake; tena hawezi kufanya zambi, maana Mungu ni baba yake. Hii ndiyo njia inayoonyesha wazi tofauti kati ya watoto wa Mungu na watoto wa Shetani. Mutu asiyetenda mambo ya haki au asiyemupenda ndugu yake si mutoto wa Mungu. Kwa maana huu ndio ujumbe muliosikia tangia mbele: tupendane sisi kwa sisi. Tusikuwe kama Kaina aliyekuwa wa yule Mwovu, akamwua ndugu yake. Yeye alimwua kwa sababu gani? Kwa sababu matendo yake yalikuwa mabaya na ya ndugu yake yalikuwa ya haki. Basi wandugu zangu, musishangae kama watu wa dunia hii wakiwachukia ninyi. Sisi tunajua kwamba tumeponyoka lufu na kupata uzima kwa sababu tunawapenda wandugu zetu. Mutu asiyekuwa na upendo ni kama mufu. Kila mutu anayemuchukia ndugu yake ni mwuaji, nanyi munajua kwamba mwuaji yeyote hana uzima wa milele ndani yake. Sisi tumetambua upendo kwa njia hii: Yesu Kristo alitoa uzima wake kwa ajili yetu. Nasi vilevile tunapaswa kutoa uzima wetu kwa ajili ya wandugu zetu. Mutu akiwa na mali ya dunia hii naye akimwona ndugu yake katika hitaji, lakini hataki kumusikilia huruma, mutu yule anaweza kusema kwamba anamupenda Mungu? Watoto wangu, upendo wetu usikuwe wa masemi tu; lakini unapaswa kuwa upendo wa kweli na unaoonekana kwa matendo. Kwa njia hii tutatambua kwamba sisi ni watu wa ukweli, na mioyo yetu itatulia mbele ya Mungu. Kwa maana hata kama zamiri yetu inatuhukumu, tunajua kwamba mafikiri ya Mungu yanapita zamiri yetu, naye anajua yote. Wapendwa wangu, zamiri yetu isipotuhukumu, sisi tuko na tumaini mbele ya Mungu. Nasi tunapokea jambo lolote tunaloomba kwake, kwa sababu tunatii amri zake na kutenda mambo yanayomupendeza. Amri yake ndiyo hii tuamini jina la Mwana wake Yesu Kristo na tupendane sisi kwa sisi kama vile Kristo alivyotuamuru. Mutu anayetii amri za Mungu anakaa ndani yake, na Mungu anakaa ndani ya yule mutu. Tunatambua kwamba Mungu anakaa ndani yetu kwa njia ya Roho Mutakatifu aliyetupatia. Wapendwa wangu, musimwaminie kila mutu anayesema kwamba yuko na Roho wa Mungu, lakini mumupime kwa kuhakikisha kama roho yule anatoka kwa Mungu. Kwa maana manabii wengi wa uongo wametokea katika dunia. Mutatambua Roho wa Mungu kwa njia hii: kila mutu anayesadiki kwamba Yesu Kristo amekuja katika hali ya kimutu yuko na Roho wa Mungu. Lakini mutu yeyote asiyemusadikia Yesu hana Roho anayetoka kwa Mungu. Mutu yule yuko na roho ya mupinga Kristo. Ninyi mumekwisha kusikia kwamba roho yule atakuja, na sasa amekwisha kuja katika dunia. Lakini ninyi, watoto wangu, muko watoto wa Mungu, nanyi mumewashinda manabii wa uongo; maana roho anayekaa ndani yenu ni mwenye uwezo kuliko yule anayekaa ndani ya watu wa dunia. Manabii wa uongo ni watu wa dunia, ndiyo maana wanasema mambo ya kidunia nao watu wa dunia wanawasikiliza. Lakini sisi ni watu wa Mungu. Mutu anayemujua Mungu anatusikiliza; yule asiyemujua Mungu hatusikilizi. Basi ni kwa njia hii tunaweza kutambua tofauti kati ya Roho wa ukweli na roho ya udanganyifu. Wapendwa wangu, tupendane, kwa maana upendo unatoka kwa Mungu. Kila mutu anayekuwa na upendo ni mutoto wa Mungu naye anamujua Mungu. Mutu asiyekuwa na upendo hamujui Mungu kwa maana Mungu ni upendo. Hii ndiyo namna Mungu alivyoonyesha upendo wake kwetu: alimutuma Mwana wake wa pekee katika dunia kusudi kwa njia yake tupate uzima wa milele. Na huu ndio upendo: si kwamba sisi tulimupenda Mungu, lakini kwamba ni yeye ndiye aliyetupenda hata akatuma Mwana wake kama vile sadaka iliyotolewa kwa ajili ya usamehe wa zambi zetu. Wapendwa wangu, ikiwa Mungu alitupenda sisi namna ile, sisi vilevile tunapaswa kupendana. Hakuna hata mutu aliyekwisha kumwona Mungu wakati wowote. Tukipendana sisi kwa sisi, Mungu anaungana nasi na upendo wake unakamilika ndani yetu. Kwa njia hii tunatambua kwamba sisi tunakaa ndani ya Mungu, naye anakaa ndani yetu: yeye ametupatia Roho wake. Na sisi tumeona na kushuhudia kwamba Baba amemutuma Mwana wake kuwa Mwokozi wa dunia. Kila mutu anayesema kwamba Yesu ni Mwana wa Mungu, Mungu anaungana naye, na mutu yule anaungana na Mungu. Na sisi tumejua na kuamini upendo Mungu anaokuwa nao kwetu. Mungu ni upendo. Yule anayeishi katika upendo anaungana na Mungu, na Mungu anaungana naye. Hivi upendo umekamilishwa ndani yetu, kusudi tupate kuwa na tumaini kwa Siku ile ya hukumu. Kwa sababu maisha yetu katika dunia hii yanafanana na maisha ya Yesu Kristo. Katika upendo hakuna woga, lakini upendo kamili unaondoa woga wote. Maana yule anayekuwa na woga hakamiliki katika upendo kwa sababu woga unaonyesha hali ya kuhukumiwa. Sisi tuko na upendo kwa sababu Mungu ndiye aliyetupenda wa kwanza. Kama mutu akisema “Ninamupenda Mungu,” naye anamuchukia ndugu yake, yeye ni mwongo. Kwa maana yule asiyemupenda ndugu yake anayemwona, hawezi kumupenda Mungu asiyemwona. Basi hii ndiyo amri tuliyopewa na Kristo: yule anayemupenda Mungu anapaswa kumupenda ndugu yake vilevile. Mutu yeyote anayeamini kwamba Yesu ndiye Kristo, yeye ni mutoto wa Mungu; na kila mutu anayemupenda baba anamupenda mwana wake vilevile. Hii ndiyo namna tunavyojua kwamba tunawapenda watoto wa Mungu: kwa kumupenda Mungu na kushika amri zake. Kwa maana kumupenda Mungu ni kutii amri zake. Na amri zake si ngumu, kwa sababu kila mutoto wa Mungu anashinda dunia. Tunashinda dunia kwa njia ya imani yetu. Ni nani anayeshinda dunia? Ni yule anayeamini kwamba Yesu ni Mwana wa Mungu. Yesu Kristo ndiye aliyekuja kwa maji ya ubatizo wake na kwa damu ya kufa kwake. Hakukuja na maji tu, lakini pamoja na maji na damu. Naye Roho ndiye anayeshuhudia mambo yale kwa sababu Roho ni wa ukweli. Maana kuna washuhuda watatu: Roho, maji na damu, nao watatu wanapatana kwa ushuhuda mumoja. Kama tunakubali ushuhuda wa wanadamu, ushuhuda wa Mungu ni wenye maana zaidi, na ni huu ndio ushuhuda Mungu aliotoa juu ya Mwana wake. Yule anayemwamini Mwana wa Mungu yuko na ushuhuda huu ndani yake. Lakini yule asiyemwamini Mungu, amemufanya Mungu kuwa mwongo, maana hakuaminia ushuhuda Mungu aliotoa juu ya Mwana wake. Na huu ndio ushuhuda ule: Mungu alitupatia uzima wa milele na uzima huu unapatikana kwa njia ya Mwana wake. Yule anayekuwa na Mwana wa Mungu yuko na uzima ule, lakini yule asiyekuwa na Mwana wa Mungu hana uzima. Ninawaandikia maneno yale, ninyi wenye kuamini kwa jina la Mwana wa Mungu, mupate kujua kwamba muko na uzima wa milele. Nasi tuko na tumaini hili mbele ya Mungu: tunajua kwamba atatusikiliza tukimwomba kitu chochote kufuatana na mapenzi yake. Basi, ikiwa tunajua kwamba anatusikiliza wakati tunapomwomba, tunajua vilevile kwamba anatupatia chochote tulichomwomba. Mutu akimwona ndugu yake anafanya zambi isiyoleta kifo, anapaswa kumwombea kwa Mungu, Mungu atamupa mutu yule uzima. Jambo hili linaelekea wale wanaotenda zambi isiyoleta kifo. Maana kuna zambi inayoleta kifo lakini sisemi kama ataomba juu ya hiyo. Kila tendo lisilokuwa la haki ni zambi, lakini kuna zambi isiyoleta kifo. Tunajua kwamba kila mutoto wa Mungu hafanyi zambi, kwa maana Mwana wa Mungu anamulinda, wala yule Mwovu hawezi kumugusa. Tunajua kwamba sisi ni watoto wa Mungu ingawa dunia yote inatawaliwa na yule Mwovu. Tunajua vilevile kwamba Mwana wa Mungu amekwisha kuja, naye ametupatia ufahamu tupate kumujua Mungu anayekuwa wa kweli. Nasi tunaungana na yule Mungu anayekuwa wa kweli kwa njia ya Mwana wake Yesu Kristo. Huyu ndiye Mungu wa kweli na uzima wa milele. Watoto wangu wapendwa, muepuke kuabudu sanamu za miungu. Barua hii inatoka kwangu mimi muzee. Ninakuandikia wewe mama uliyechaguliwa na Mungu, pamoja na watoto wako ninaowapenda hakika. Wala si mimi peke tu ninayewapenda, lakini vilevile wale wote wanaojua ule ukweli wanawapenda ninyi, kwa sababu ukweli huu unakaa ndani yetu nao utakuwa pamoja nasi hata milele. Mungu Baba pamoja na Yesu Kristo, Mwana wa Baba, watatujalia neema, huruma na amani katika ukweli na upendo. Nilifurahi sana kuona kwamba wamoja kati ya watoto wako wanaishi katika ukweli kama vile Baba alivyotuamuru. Na sasa Mama, ninakusihi: tupendane. Basi hii si amri mupya ninayokuandikia, lakini ni amri ile tuliyopokea tangu mwanzo. Na upendo ni kuishi katika kutii amri za Mungu. Hii ndiyo ile amri muliyoisikia tangu mwanzo: muishi katika upendo. Kwa maana wadanganyifu wengi wametokea katika dunia. Watu hawa hawakubali kwamba Yesu Kristo amekuja katika mwili wa kimutu. Yule asiyekubali vile ni mudanganyifu na mupinga Kristo. Basi, mujiangalie wenyewe, kusudi musipoteze matunda ya kazi yenu, lakini mupokee zawadi kamili. Kila mutu atakayeenda mbali na asiyedumu katika mafundisho ya Kristo, mutu yule hashirikiani na Mungu. Lakini yule anayedumu katika mafundisho yale, anashirikiana na Baba na Mwana vilevile. Mutu akikuja kwenu, naye asipowafundisha mafundisho haya, musimukaribishe ndani ya nyumba yenu, wala musimusalimie; maana mwenye kumusalimia anashirikiana naye katika matendo yake mabaya. Nina maneno mengi ya kuwaambia, lakini sitaki kuyaandika ndani ya barua. Ninatumaini nitawatembelea na kusemezana pamoja nanyi uso kwa uso, kusudi tupate kujazwa na furaha kabisa. Upokee salamu za watoto wa dada yako aliyechaguliwa na Mungu. Barua hii inatoka kwangu mimi muzee. Ninakuandikia wewe Gayo, mupendwa wangu, ninayekupenda hakika. Mupendwa wangu, ninakutakia maendeleo mazuri katika kila jambo; ninakutakia afya njema katika mwili, kama vile unavyokuwa nayo katika roho. Nilifurahi sana wakati wandugu wamoja walipofika na kunielezea juu ya ukweli unaokuwa ndani yako na kwamba unaishi katika ukweli. Hakuna jambo linalonifurahisha kuliko lile la kusikia kwamba watoto wangu wanaishi katika ukweli. Mupendwa wangu, wewe ni mwaminifu kwa kazi unayofanya kwa ajili ya wandugu, hata kwa wale wanaokuwa wageni. Wandugu hawa walishuhudia upendo wako mbele ya kanisa. Ninakusihi uwasaidie wapate kuendelea na safari yao kwa namna inavyomupendeza Mungu. Kwa maana hawa walianza safari yao kwa ajili ya kazi ya Kristo bila kupokea musaada wowote toka kwa watu wasioamini. Basi sisi tunapaswa kuwasaidia watu kama hawa tupate kushiriki pamoja nao katika kazi ya kutangaza ukweli. Nimeandikia kanisa maneno machache lakini Diotrefe, anayependa kuwa musimamizi wao, anakataa kututii. Kwa sababu hiyo wakati nitakapokuja, nitaonyesha wazi mambo yote anayotenda akitusingizia sisi maneno mabaya. Lakini hatosheki na mambo yale, yeye mwenyewe anakataa kukaribisha wandugu wale wanaokuwa katika safari. Na wale wanaotaka kuwakaribisha, anawakataza na kuwafukuza katika kanisa. Mupendwa wangu, usifuate mufano mubaya, lakini ufuate mufano muzuri. Mutu anayetenda mema ni mutoto wa Mungu; lakini anayetenda mabaya hashirikiani na Mungu. Watu wote wameshuhudia Demetrio vizuri; hakika ukweli wenyewe unahakikisha jambo lile. Sisi vilevile tunamushuhudia, nawe unajua kwamba ushuhuda wetu ni wa kweli. Nina maneno mengi ya kukuambia lakini sitaki kuyaandika ndani ya barua. Ninatumaini kwamba nitakuona sasa hivi na wakati ule tutasemezana pamoja uso kwa uso. Ninakutakia amani. Warafiki zako wanakusalimia. Utusalimie warafiki zetu, kila mutu kwa upekee. Barua hii inatoka kwangu mimi Yuda, mutumishi wa Yesu Kristo na ndugu wa Yakobo. Ninawaandikia ninyi mulioitwa na Mungu Baba na munaoishi katika upendo wake na kulindwa kwa ajili ya Yesu Kristo. Ninawatakia huruma, amani na upendo kwa uwingi. Wapendwa wangu, wakati nilipokuwa nikifanya bidii sana ya kuwaandikia juu ya wokovu tunaoshiriki wote pamoja, nikaona sherti niwaandikie na kuwaonya mupate kutetea imani ile Mungu aliyotoa mara moja tu kwa watu wake. Maana kuna watu wasiomuheshimu Mungu waliojiingiza kwa siri kati yetu. Watu hawa wanapotosha ujumbe wa neema ya Mungu wetu kusudi wapate kufanya uasherati na kumukana Yesu Kristo, anayekuwa peke yake Kiongozi na Bwana wetu. Tangia zamani Maandiko Matakatifu yamejulisha hukumu ile itakayowapata watu hawa. Ijapokuwa mumekwisha kujua kabisa mambo haya yote, ninataka kuwakumbusha namna Bwana alivyowaokoa Waisraeli kutoka katika inchi ya Misri, lakini kisha, akawaangamiza wale waliokataa kuamini. Mukumbuke vilevile wamalaika wale waliokosa kulinda vema cheo chao, lakini wakaacha makao yao: Mungu akawaweka katika nafasi ya giza, wakifungwa minyororo ya milele kwa kungojea Siku ile ya hukumu. Mukumbuke vilevile watu wa Sodoma na Gomora na wa miji iliyokuwa kandokando wanaokuwa sawasawa na wamalaika hawa. Walifanya uasherati na mambo ya kimwili yasiyokuwa ya kawaida ya asili. Watu hawa wanapokea hukumu ya moto wa milele kuwa mufano wazi kwa watu wote. Hata hivi, watu hawa vilevile wanafanana nao; maono yao yanawasukuma kuchafua miili yao na kuzarau mamlaka ya Mungu na kutukana viumbe vitukufu vya mbinguni. Hata Mikaeli, malaika mukubwa, aliposhindana na kubishana na Shetani juu ya maiti ya Musa, hakusubutu kumuhukumu kwa matusi, lakini alisema: “Bwana mwenyewe akukaripie.” Lakini watu hawa wanasema vibaya juu ya mambo wasiyoyafahamu; na mambo wanayoyajua kwa tabia yao kama nyama wasiokuwa na akili, ndiyo yale yanayowaangamiza. Ole kwao! Maana wamefuata njia ya Kaina. Kwa ajili ya kupata mali wameanguka katika kosa Balama alilofanya. Wameangamia kwa sababu wameasi kama vile Kora alivyoasi. Kufika kwao kunaleta machafuko katika karamu zenu za upendo. Wanakula na kushiba pamoja nanyi pasipo haya yoyote. Wao ni kama mawingu yanayopeperushwa na upepo pasipo kuleta mvua. Wao ni kama miti isiyozaa matunda hata wakati wa mavuno; ni miti iliyoongolewa na kufa kabisa. Wanafanana na zoruba kubwa ya bahari na matendo yao ya haya yanaonekana kama pofu ya zoruba. Wanafanana vilevile na nyota zinazotangatanga; Mungu amekwisha kuwawekea nafasi katika giza kubwa kwa milele. Ni Enoki, mutu wa kizazi cha saba tangu Adamu, ndiye aliyetabiri zamani juu yao, akisema: “Musikilize, Bwana atakuja pamoja na maelfu na maelfu ya wamalaika zake watakatifu. Atakuja kuwahukumu wote na kuwaazibu watu wabaya wasiomwogopa Mungu, kwa ajili ya matendo yao yote mabaya waliyotenda, na kwa ajili ya maneno yote mabaya wenye zambi hawa waliyosema juu yake.” Watu hawa wanaendelea kunungunika na kuteta wengine. Wanaishi kufuatana na tamaa zao mbaya. Wanasema maneno ya majivuno na kujipendekeza kwa watu kusudi wapate faida toka kwao. Lakini ninyi wapendwa wangu, mukumbuke maneno yaliyosemwa zamani na mitume wa Bwana wetu Yesu Kristo. Wao waliwaambia: “Katika siku za mwisho, kutakuja watu watakaowachekelea, wakiishi kwa kufuata tamaa zao mbaya.” Watu hawa ndio wanaoleta matengano; wanatawaliwa na tabia za kimwili nao hawana Roho wa Mungu. Lakini ninyi wapendwa wangu, muendelee kusimama imara katika imani yenu inayokuwa takatifu sana, mukiomba kwa uwezo wa Roho Mutakatifu. Mudumu katika upendo wa Mungu, mukimungojea Bwana wetu Yesu Kristo, atakayewapa ninyi uzima wa milele kwa huruma yake. Mukuwe na moyo wa huruma kwa wale wanaokuwa na mashaka: muwaokoe, mukiwaopoa toka katika moto. Muwasikilie vilevile wengine huruma, lakini kwa woga, mukichukia hata nguo zao zilizochafuliwa na tamaa zao mbaya. Basi yeye anayeweza kuwalinda kusudi musianguke, na kuwasimamisha ninyi mbele ya utukufu wake pasipo kilema na kwa furaha kubwa, yeye anayekuwa Mungu peke yake, Mwokozi wetu, asifiwe na kuwa na ukubwa, uwezo na mamlaka, kwa njia ya Yesu Kristo Bwana wetu, tangia zamani za kale, sasa na hata milele! Amina. Hizi ni habari za mambo yaliyofunuliwa na Yesu Kristo. Kristo alipata ufunuo huu kutoka kwa Mungu, kusudi awaonyeshe watumishi wake mambo yanayopaswa kutokea kisha kidogo. Kristo alimutuma malaika wake kwa kumujulisha mutumishi wake Yoane mambo yale. Naye Yoane alishuhudia kwamba mambo yote aliyoona yanaelekea Neno la Mungu na ukweli ulioshuhudiwa na Yesu Kristo. Heri yule anayesoma na wale wanaosikia maneno hayo ya unabii na kushika yale yaliyoandikwa ndani ya kitabu hiki, kwa maana wakati wa kutimia kwa mambo haya unakaribia. Ni mimi Yoane ninayewaandikia ninyi makanisa saba munaokuwa katika jimbo la Azia. Ninawatakia neema na amani kutoka kwa Mungu anayekuwa, aliyekuwa na anayekuja, na kutoka kwa roho saba wanaokuwa mbele ya kiti chake cha kifalme, na kutoka kwa Yesu Kristo. Yeye ni mushuhuda mwaminifu, naye ndiye wa kwanza aliyefufuliwa, vilevile yeye ni mukubwa wa wafalme wa dunia. Yeye anatupenda na ametukomboa toka katika zambi zetu kwa njia ya damu yake. Hivi akatupatia ufalme wa kikuhani kusudi tumutumikie Mungu Baba yake. Yesu Kristo atukuzwe na kuwa na uwezo kwa milele na milele. Amina. Angalia, yeye anakuja katikati ya mawingu! Kila mutu atamwona, hata wale waliomutoboa kwa mukuki. Na kwa sababu yake mataifa yote ya dunia yatalalamika kwa huzuni. Hakika ni vile! Amina. Bwana Mungu Mwenye Uwezo anasema: “Mimi ni Alfa na Omega.” Ni yeye anayekuwa, aliyekuwa na anayekuja. Mimi ni ndugu yenu Yoane. Kwa njia ya kuungana na Yesu, ninashirikiana nanyi katika mateso, katika ufalme wake na katika kuvumilia. Mimi nilikuwa nimepelekwa katika kisanga kinachoitwa Patimo, kwa sababu nilihubiri Neno la Mungu na ukweli ulioshuhudiwa na Yesu. Siku moja ya kumwabudu Bwana, nikashikwa na Roho wa Mungu, nikasikia sauti kubwa, inayolia kama baragumu, ikisema: “Andika katika kitabu mambo unayoona, na ukitume kwa makanisa ya miji saba: Efeso, Smurna, Pergamo, Tuatera, Sardi, Filadelfia na Laodikia.” Basi nikageuka kusudi nione yule aliyesema nami. Na wakati nilipogeuka nikaona vinara saba vya taa vilivyotengenezwa na zahabu. Na katikati ya vile vinara saba, nikaona kiumbe kimoja kinachofanana na Mwana wa Mutu. Naye alikuwa amevaa kanzu ndefu inayofika hata kwenye miguu yake na mukaba wa zahabu katika kifua chake. Nywele zake zilikuwa nyeupe sana kama pamba na kama barafu, macho yake yalimetameta kama ndimi za moto. Miguu yake ilingaa kama shaba iliyosafishwa vizuri sana katika furu ya moto, na sauti yake ilinguruma kama maporomoko ya maji mengi. Alikuwa ameshika nyota saba katika mukono wake wa kuume. Ndani ya kinywa chake mulitoka upanga wenye makali ngambo zote mbili, uso wake ulingaa sana kama jua wakati linapopiga vikali sana. Wakati nilipomwona, nikaanguka chini kwa rafla mbele yake kama vile mufu. Lakini akaweka mukono wake wa kuume juu yangu na kusema: “Usiogope! Mimi ni wa kwanza na wa mwisho. Mimi ni mwenye uzima. Nilikuwa nimekufa, lakini sasa mimi niko muzima kwa milele na milele. Niko na mamlaka juu ya lufu na kuzimu. Basi uandike mambo unayoona, na mambo yanayokuwa sasa na yale yatakayotokea nyuma. Hii ndiyo maana ya lile fumbo juu ya zile nyota saba ulizoona katika mukono wangu wa kuume, na vile vinara saba vya zahabu: zile nyota saba ni wamalaika wa makanisa saba na vile vinara saba ni yale makanisa saba. “Umwandikie malaika wa kanisa la Efeso hivi: “Ujumbe huu unatoka kwa yule anayeshika nyota saba katika mukono wake wa kuume na anayetembea katikati ya vinara saba vya taa vya zahabu. Ninajua matendo yako na taabu yako na uvumilivu wako. Ninajua kwamba hauwezi kuwakubali watu waovu. Umewapima wale wanaojiita mitume, kumbe si mitume, nawe ukatambua kwamba ni wasema uongo. Wewe ni muvumilivu; umeteswa kwa ajili ya jina langu, lakini haukuregea. Lakini niko na neno moja juu yako: wewe hauna tena upendo kwangu kama vile mbele. Basi kumbuka jinsi ulivyokuwa ulipokuwa haujaanguka, ugeuke toka zambi zako na kurudilia yale matendo yako ya kwanza. Kama usipogeuka toka zambi zako, nitakuja kwako na kuongoa kinara chako toka pahali pake. Lakini uko na neno hili zuri: unachukia matendo ya Wanikolayi kama vile ninavyoyachukia. “Mwenye kuwa na masikio, asikie vizuri vile Roho anavyoyaambia makanisa! “Yule atakayeshinda nitamupa ruhusa ya kula matunda ya muti wa uzima unaokuwa katika bustani ya Mungu! “Umwandikie malaika wa kanisa la Smurna hivi: “Ujumbe huu unatoka kwa yule anayekuwa wa kwanza na wa mwisho, aliyekuwa amekufa lakini sasa ni muzima. Ninajua mateso yako na umasikini wako, lakini wewe ni tajiri! Vilevile ninajua jinsi unavyotukanwa na wale wanaojidai kuwa Wayuda lakini si Wayuda; wao ni kikundi cha wenye kuabudu Shetani! Usiogope mateso utakayopata. Sikiliza, Shetani atawajaribu kwa njia ya kuwatia wamoja wenu katika kifungo, nanyi mutateseka kwa muda wa siku kumi. Lakini ukuwe mwaminifu mpaka kufa, nami nitakupatia taji ya uzima. “Mwenye kuwa na masikio, asikie vizuri vile Roho anavyoambia makanisa! “Yule atakayeshinda hatapatwa na kifo cha pili. “Umwandikie malaika wa kanisa la Pergamo hivi: “Ujumbe huu unatoka kwa yule anayekuwa na upanga wenye makali ngambo zote mbili. Ninajua pahali pale unapokaa, ile ndiyo nafasi ya utawala wa Shetani. Wewe unashikamana na jina langu, wala haukuikana imani unayokuwa nayo kwangu, hata wakati Antipa, mushuhuda wangu mwaminifu, alipouawa kati yenu kule kwenye makao ya Shetani. Lakini niko na neno hili juu yako: kati yako kuna watu wamoja wanaoshika mafundisho ya Balama. Huyu ndiye aliyemufundisha Balaka kwamba awapime Waisraeli, kusudi wakule vyakula vya kutambikia sanamu za miungu na kufanya uasherati. Na zaidi ya hii kati yako kuna watu wanaoshika mafundisho ya Wanikolayi vilevile. Basi ugeuke toka zambi zako, kwa maana kama si vile nitakuja kwako upesi, nami nitapigana na watu wale kwa upanga unaotoka ndani ya kinywa changu. “Mwenye kuwa na masikio, asikie vizuri vile Roho anavyoyaambia makanisa! “Yule atakayeshinda, nitamupa ile mana iliyofichwa. Na nitamupa vilevile jiwe dogo jeupe, na juu yake kumeandikwa jina jipya ambalo hakuna mutu yeyote anayelijua, isipokuwa tu yule anayelipewa. “Umwandikie malaika wa kanisa la Tuatera hivi: “Ujumbe huu unatoka kwa Mwana wa Mungu, anayekuwa na macho yanayometameta kama ndimi za moto, na miguu inayongaa kama shaba iliyosafishwa vizuri sana. Ninajua matendo yako, upendo wako, imani yako, kazi yako na uvumilivu wako. Ninajua kwamba sasa unajitolea kwa kunitumikia kuliko mbele. Lakini niko na neno hili juu yako: unamuvumilia yule mwanamuke Yezebeli, anayejiita kuwa nabii wa Mungu. Yeye anawapotosha watumishi wangu akiwafundisha kufanya uasherati na kula nyama za kutambikia sanamu za miungu. Nimemwachia wakati wa kugeuka toka zambi zake, lakini hataki kuacha uasherati wake. Basi nitamupiga kwa ugonjwa na kuleta mateso makubwa vilevile kwa wale wanaozini pamoja naye ikiwa hawaachi matendo yao. Nitawaua wafuasi wake. Na hivi makanisa yote yatajua kwamba mimi ndiye ninayechunguza mioyo ya watu na mafikiri yao. Vilevile yatajua kwamba mimi nitamulipa kila mumoja wenu kufuatana na matendo yake. “Lakini ninyi watu wengine wa kanisa la Tuatera musiofuata hayo mafundisho ya Yezebeli, na ambao hamujui ile wanayoita ‘Siri za Shetani’, ninawaambia ninyi kama sitawabebesha muzigo mwingine. Lakini ninawaomba tu mushikamane na kile munachokuwa nacho mpaka nitakapokuja. Na yule atakayeshinda na kuendelea kufuata mapenzi yangu mpaka mwisho, nitamupa mamlaka ya kutawala mataifa. Atayatawala kwa fimbo ya chuma na kuyaponda kama vile mutungi, akiwa na uwezo sawa ule uliopewa na Baba yangu. Na zaidi ya ile nitamupa nyota ya asubui. “Mwenye kuwa na masikio, asikie vizuri vile Roho anavyoyaambia makanisa! “Umwandikie malaika wa kanisa la Sardi hivi: “Ujumbe huu unatoka kwa yule anayekuwa na roho zile saba za Mungu na zile nyota saba. Ninajua matendo yako, hakika wewe umekwisha kufa ingawa unajulikana kuwa muzima. Amuka! Uimarishe kile kinachobaki kinachokaribia kufa, kwa maana nimeona kwamba matendo yako si makamilifu mbele ya Mungu wangu. Basi ukumbuke mafundisho uliyopokea na yale uliyosikia. Uyashike na kugeuka toka zambi zako. Kama usipokesha, nitakuja kama mwizi, wala hautajua saa nitakapokuja kwako. Lakini ungali na watu wachache kule Sardi wasiochafua nguo zao. Wale ndio watakaotembea pamoja nami wakivaa nguo nyeupe kwa sababu wanastahili. Yule atakayeshinda atavalishwa nguo nyeupe, nami sitafuta jina lake kati ya majina yanayoandikwa katika kitabu cha uzima. Nami nitamutetea mbele ya Baba yangu na mbele ya wamalaika zake. “Mwenye kuwa na masikio, asikie vizuri vile Roho anavyoyaambia makanisa! “Umwandikie malaika wa kanisa la Filadelfia hivi: “Ujumbe huu unatoka kwa yule anayekuwa mutakatifu na mwenye ukweli, anayekuwa na ufunguo wa mufalme Daudi, anayefungua mulango wala hakuna anayeweza kuufunga, anayefunga wala hakuna anayeweza kuufungua. Ninajua matendo yako. Ninajua kwamba wewe hauna uwezo mwingi, lakini umeshika neno langu, nawe haukukana jina langu. Basi nimefungua mulango wazi mbele yako, wala hakuna anayeweza kuufunga. Angalia, nitakupa watu wa kikundi chenye kuabudu Shetani, ndio wale wasema uongo wanaojidai kwamba wao ni Wayuda, lakini ni wadanganyifu. Hakika nitawalazimisha kupiga magoti mbele yako, nao watajua ya kuwa mimi ninakupenda. Kufuatana na vile ulivyojichunga katika uvumilivu sawa nilivyokuagiza, mimi vilevile nitakuchunga na hasara wakati itakapokuja katika dunia yote kwa kuwajaribu wakaaji wake. Ninakuja upesi. Shika sana kile unachokuwa nacho, kusudi mutu yeyote asinyanganye taji yako ya ushindi. Yule atakayeshinda nitamufanya kuwa nguzo katika hekalu la Mungu wangu, naye hatatoka tena mule. Na zaidi ya ile nitaandika juu yake jina la Mungu wangu na jina la muji wa Mungu wangu, ndio Yerusalema mupya, utakaoshuka toka mbinguni kwa Mungu wangu. Nitaandika vilevile juu yake jina langu jipya. “Mwenye kuwa na masikio, asikie vizuri vile Roho anavyoyaambia makanisa. “Umwandikie malaika wa kanisa la Laodikia hivi: “Ujumbe huu unatoka kwa yule anayeitwa ‘Amina’, mushuhuda mwaminifu, mwenye ukweli, na musingi wa viumbe vyote vya Mungu. Ninajua matendo yako: wewe si baridi wala si moto. Afazali ungekuwa baridi tu au moto tu. Lakini sasa kwa sababu wewe ni mwenye uvuguvugu, ni kusema hauko baridi wala moto, nitakutapika kutoka katika kinywa changu. Wewe unajidai kwamba uko tajiri mwenye mali mengi, wala haukosewi kitu. Lakini haujui kwamba wewe ni mukosefu, mwenye taabu, masikini, kipofu na mwenye kuwa uchi. Kwa hiyo ninakushauria kununua kwangu zahabu iliyosafishwa kwa moto, kusudi upate kuwa tajiri. Vilevile ununue nguo nyeupe, upate kuvaa na kufunika uchi wako unaokuletea haya. Tena ununue dawa ya kutia ndani ya macho yako, kusudi upate kuona. Mimi ninawaonya na kuwaazibu wote ninaowapenda. Basi ufanye nguvu, ugeuke toka katika zambi. Sikiliza, ninasimama kwenye mulango na ninapiga hodi. Kama mutu akisikia sauti yangu na kunifungulia, nitaingia kwake, nami nitakula pamoja naye, na yeye atakula pamoja nami. Yule atakayeshinda, nitamwikalisha karibu nami kwenye kiti changu cha kifalme, kama vile mimi nilivyoshinda na kuikaa karibu na Baba yangu kwenye kiti chake cha kifalme. “Mwenye kuwa na masikio, asikie vizuri vile Roho anavyoyaambia makanisa.” Nyuma ya mambo hayo nilipata maono mengine. Niliona mulango mumoja umefunguliwa wazi mbinguni. Halafu ile sauti niliyosikia mara ya kwanza, iliyolia kama baragumu, ikaniambia: “Panda huku, nami nitakuonyesha mambo yanayopaswa kutokea nyuma ya hayo ya mbele.” Na mara moja nikashikwa na Roho wa Mungu. Nikaona kiti cha kifalme kimewekwa kule mbinguni na mutu mumoja alikuwa akiikaa juu ya kiti kile. Mutu yule aliangaa kama mawe ya bei kali ya yaspi na sardio. Kiti kile cha kifalme kilikuwa kimezungukwa na upindi wa mvua uliongaa kama jiwe la zumaridi. Na kiti kile kilikuwa kimezungukwa na viti vingine makumi mbili na vine vya kifalme na juu ya viti vile kulikuwa kumeikaa wazee makumi mbili na wane. Wale wazee walikuwa wamevaa nguo nyeupe na juu ya kichwa chao kulikuwa taji za zahabu. Umeme ulipiga tokea katika kiti kile, na makelele na ngurumo ya radi vilisikilika. Mbele ya kiti kile kulikuwa kukiwaka mienge saba, na hizo ndizo zile roho saba za Mungu. Tena mbele ya kiti kile kulionekana kama bahari ya kioo, kulingaa sana kama kilauri. Kile kiti cha kifalme kilikuwa kimezungukwa pande zote na viumbe vine vya ajabu, vyenye kujaa macho mbele na nyuma. Kiumbe cha kwanza kilifanana na simba, kiumbe cha pili kilifanana na mwana-ngombe na kiumbe cha tatu kilifanana na mutu na kiumbe cha ine kilifanana na tai anayeruka. Na kila kimoja cha viumbe vya ajabu kilikuwa na mabawa sita yenye kujaa macho ndani na inje. Navyo viliimba muchana na usiku bila kuchoka, vikisema: “Mutakatifu, mutakatifu, mutakatifu ni Bwana wetu, Mungu Mwenye Uwezo, aliyekuwa, anayekuwa na anayekuja.” Vile viumbe vine vya ajabu viliimba kwa kumutukuza, kumuheshimia na kumushukuru yule aliyeikaa juu ya kiti cha kifalme, yule anayeishi kwa milele na milele. Kila mara vilipofanya vile, wale wazee makumi mbili na wane waliinama uso mpaka chini mbele ya yule anayeikaa juu ya kiti cha kifalme, wakimwabudu huyo anayeishi kwa milele na milele. Nao walikuwa wakikuja kuweka taji zao mbele ya kiti chake, na kusema: “Bwana wetu na Mungu wetu, wewe unastahili utukufu, heshima na uwezo, kwa maana wewe ndiwe uliyeumba vitu vyote; vile vimeumbwa na kupata kuwa kutokana na mapenzi yako.” Kisha nikaona kizingo cha karatasi katika mukono wa kuume wa yule aliyeikaa juu ya kiti cha kifalme. Kizingo kile kilikuwa kimeandikwa ngambo na ngambo na kufungwa kwa vifundo saba vya mihuri. Nikaona malaika mwenye uwezo aliyekuwa akitangaza hivi kwa sauti kubwa: “Ni nani anayestahili kuvunja vile vifundo vya mihuri na kufungua kizingo kile?” Lakini hakukuwa hata mutu mbinguni, wala katika dunia, wala katika kuzimu aliyeweza kufungua kizingo kile na kuangalia ndani yake. Nami nikalia sana, kwa sababu hakukuonekana mutu aliyestahili kufungua kizingo wala kuangalia ndani yake. Basi mumoja kati ya wale wazee akaniambia: “Usilie. Angalia, simba wa kabila la Yuda, wa uzao wa mufalme Daudi, amepata ushindi. Yeye anaweza kuvunja vile vifundo saba vya muhuri vya kizingo na kukifungua.” Halafu nikaona Mwana-Kondoo akisimama katikati ya kiti cha kifalme chenye kuzungukwa na vile viumbe vine vya ajabu na wale wazee, naye alionekana kama amechinjwa. Alikuwa na pembe saba na macho saba; ndizo roho saba za Mungu zilizotumwa katika dunia yote. Yule Mwana-Kondoo akajongea na kukamata kizingo kutoka mukono wa kuume wa yule aliyeikaa juu ya kiti cha kifalme. Wakati alipokuwa amekwisha kukamata kizingo, vile viumbe vine vya ajabu na wale wazee makumi mbili na wane wakainama uso mpaka chini mbele ya Mwana-Kondoo. Kila mumoja wao alikuwa na kinubi na vikombe vya zahabu vilivyojaa marasi, ndiyo maombi ya watu wa Mungu. Nao walikuwa wakiimba wimbo huu mupya wakisema: “Wewe unastahili kukamata kizingo cha karatasi, na kuvunja vifundo vya mihuri yake. Kwa sababu wewe uliuawa, na kwa njia ya damu yako, ulikomboa kwa ajili ya Mungu watu wa kila kabila, wa kila luga, wa kila jamaa na wa kila taifa. Umewapatia ufalme wa kikuhani kusudi wamutumikie Mungu wetu; nao watatawala katika dunia.” Kisha nikaangalia tena, nikasikia sauti ya wamalaika wengi wenye kuzunguka kiti cha kifalme, na viumbe vya ajabu na wazee. Hesabu yao ilikuwa maelfu na maelfu na mamilioni na mamilioni. Nao waliimba hivi kwa sauti kubwa: “Mwana-Kondoo aliyeuawa anastahili kupokea uwezo, utajiri, hekima na nguvu, heshima, utukufu na sifa!” Nikasikia vilevile viumbe vyote vinavyokuwa mbinguni, katika dunia, katika kuzimu na vile vinavyokuwa katika bahari; viumbe vyote vya ulimwengu nzima vikimwimbia: “Utukufu, heshima, sifa na nguvu milele na milele, kwa yule anayeikaa juu kiti cha kifalme na kwa Mwana-Kondoo.” Vile viumbe vine vya ajabu vilijibu: “Amina.” Na wale wazee wakainama uso mpaka chini na kuabudu. Kisha nikaona mambo haya: Mwana-Kondoo alipofungua kifundo cha muhuri wa kwanza kati ya ile mihuri saba, nikasikia kimoja kati ya vile viumbe vya ajabu kikisema hivi kwa sauti kama ya ngurumo ya radi: “Kuja!” Niliangalia, nami nikaona farasi mumoja mweupe. Na yule aliyepanda juu yake alikuwa na upindi, akapewa taji. Akatoka akiwa mushindaji na mwenye uwezo wa kuendelea kushinda. Kisha Mwana-Kondoo akafungua kifundo cha muhuri wa pili. Nikasikia kiumbe cha pili cha ajabu kikisema: “Kuja!” Kisha kukatokea farasi mwengine mwekundu. Na yule aliyepanda juu yake akapewa uwezo wa kuondoa amani katika dunia, kusudi watu wauane wao kwa wao. Naye akapewa upanga mukubwa. Mwana-Kondoo alipofungua kifundo cha muhuri wa tatu, nikasikia kiumbe cha tatu cha ajabu kikisema: “Kuja!” Niliangalia nami nikaona farasi mweusi. Na yule aliyepanda juu yake alikuwa na mizani katika mikono yake. Nikasikia kitu kama sauti iliyotokea katikati ya vile viumbe vine vya ajabu ikisema: “Kilo moja ya ngano ni mushahara wa siku nzima ya kazi, na kilo tatu ya shayiri ni mushahara wa siku nzima ya kazi, lakini usiharibu mafuta wala divai.” Wakati Mwana-Kondoo alipofungua kifundo cha muhuri wa ine, nikasikia sauti ya kiumbe cha ine cha ajabu kikisema: “Kuja!” Nikaangalia, nami nikaona farasi mwenye rangi ya kijivujivu. Na yule aliyepanda juu yake aliitwa Lufu, naye alikuwa akisindikizwa na Kuzimu. Wao wakapewa uwezo juu ya sehemu moja ya ine ya dunia kwa kuua watu kwa upanga, kwa njaa kubwa, kwa ugonjwa mukali na kwa nyama wakali. Wakati Mwana-Kondoo alipofungua kifundo cha muhuri wa tano, nikaona chini ya mazabahu, roho za watu waliouawa kwa sababu ya kutangaza Neno la Mungu na kwa sababu ya ushuhuda wao. Watu wale wakalalamika hivi kwa sauti kubwa: “Bwana mutakatifu na mwenye ukweli, mpaka wakati gani utaendelea kungojea kuwahukumu wakaaji wa dunia na kuwaazibu kwa sababu ya kuuawa kwetu?” Kila mumoja wao akapewa kanzu nyeupe, wakaambiwa wapumzike kwa muda kidogo mpaka wakati hesabu ya watumishi wenzao na wandugu watakaouawa vilevile kama wao itakapotimia. Kisha nikaona mambo haya: Mwana-Kondoo alipofungua kifundo cha muhuri wa sita, kukakuwa tetemeko kubwa la dunia; jua ikageuka kuwa nyeusi kama nguo ya kilio na mwezi ukageuka kuwa mwekundu kama damu. Nyota za mbinguni zikaanguka katika dunia kama vile matunda mabichi ya muti wa tini yanavyoanguka wakati muti wake unapotikiswa na upepo mukali. Mbingu zikaviringwa na kuwa kama kizingo cha karatasi na kutoweka. Milima yote na visanga vyote vikahamishwa kutoka kwenye nafasi yao. Wafalme wa dunia, wakubwa, wakubwa wa waaskari, watajiri, wenye uwezo, na watu wengine wote, watumwa au wenye kuwa huru wakajificha katika mapango na katikati ya mawe ya milima. Nao wakaiambia milima na mawe: “Mutuangukie na kutufunika mbali na yule anayeikaa juu ya kiti cha kifalme na mbali na kasirani ya Mwana-Kondoo. Kwa maana siku kubwa ya kasirani yao imekuja. Ni nani atakayeweza kusimama imara?” Kisha mambo yale, nikaona wamalaika wane wakisimama kwenye pembe ine za dunia, wakizuiza upepo toka pande ine za dunia, kusudi usivume juu ya dunia, wala juu ya bahari, wala juu ya muti wowote. Nikaona malaika mwingine akipanda tokea mashariki alikuwa akishika muhuri wa Mungu Mwenye Uzima. Akawalalamikia kwa sauti kubwa wale wamalaika wane waliopewa uwezo wa kuharibu dunia na bahari: “Musiharibu dunia, wala bahari, wala miti mpaka tutakapokwisha kutia chapa ya muhuri juu ya paji ya nyuso za watumishi wa Mungu wetu.” Nikasikia hesabu ya watu waliopigwa chapa ya muhuri wa Mungu ilikuwa: elfu mia moja na makumi ine na ine kutoka makabila yote ya Waisraeli. Kisha mambo haya, nikaangalia nami nikaona mukutano mukubwa sana wa watu wasioweza kuhesabiwa. Kulikuwa watu wa kila taifa, wa kila kabila, wa kila jamaa na wa kila luga. Walikuwa wakisimama mbele ya kiti cha kifalme na mbele ya Mwana-Kondoo, wakivaa kanzu nyeupe na kushika matawi ya muti wa ngazi katika mikono yao. Nao walilalamika hivi kwa sauti kubwa: “Wokovu wetu unatoka kwa Mungu wetu anayeikaa juu ya kiti cha kifalme na kwa Mwana-Kondoo!” Na wamalaika wote waliokuwa wakizunguka kile kiti cha kifalme, wazee na vile viumbe vine vya ajabu, wakainama uso mpaka chini mbele ya kiti cha kifalme, nao wakamwabudu Mungu, wakisema: “Amina! Utukufu, sifa, hekima, shukrani, heshima, uwezo, na nguvu ni vya Mungu wetu, milele na milele! Amina!” Halafu mumoja wa wale wazee akaniuliza: “Wale wanaovaa kanzu nyeupe ni watu gani nao wanatoka wapi?” Nami nikamujibu: “Bwana wangu wewe ndiwe unayejua.” Naye akaniambia: “Hawa ndio wanaotoka katika mateso makubwa. Wamesafisha kanzu zao na kuzifanya kuwa nyeupe katika damu ya Mwana-Kondoo. Ndiyo maana wanasimama mbele ya kiti cha kifalme cha Mungu, nao wanamutumikia muchana na usiku katika hekalu lake. Na yule anayeikaa juu ya kiti cha kifalme atawalinda katika hema yake. Nao hawatasikia njaa tena, wala kiu, wala jua halitawapiga tena, wala joto lolote. Kwa maana Mwana-Kondoo anayekuwa katikati ya kiti cha kifalme, atawachunga na kuwaongoza kwenye chemichemi ya maji ya uzima. Naye Mungu atawapanguza machozi yao yote.” Wakati Mwana-Kondoo alipofungua kifundo cha muhuri wa saba, kukakuwa kimya mbinguni kwa muda wa nusu ya saa. Kisha nikaona wamalaika saba wakisimama mbele ya Mungu, nao wakapewa baragumu saba. Kisha malaika mwingine akakuja kusimama karibu na mazabahu. Alikuwa akishika chetezo cha zahabu. Naye akapewa ubani mwingi kusudi autoe sadaka pamoja na maombi ya watu wote wa Mungu juu ya mazabahu ya zahabu iliyokuwa mbele ya kiti cha kifalme. Moshi wa ule ubani pamoja na maombi ya watakatifu vilipanda mbele ya Mungu toka katika mukono wa yule malaika. Kisha yule malaika akatwaa kile chetezo, akakijaza makaa ya moto toka kwenye mazabahu na kukitupa katika dunia. Na halafu kukakuwa ngurumo ya radi, makelele, umeme na tetemeko la inchi. Wale wamalaika saba waliokuwa na baragumu saba wakajitayarisha kwa kuzipiga. Malaika wa kwanza akapiga baragumu. Halafu mvua ya mawe na moto vyenye kuchanganyika na damu, vikatupwa katika dunia. Sehemu moja ya tatu ya inchi ikateketea, na sehemu moja ya tatu ya miti na majani yote vikateketea vilevile. Kisha malaika wa pili akapiga baragumu. Halafu kitu kimoja chenye kufanana na mulima mukubwa unaowaka moto kikatupwa katika bahari, na sehemu moja ya tatu ya bahari ikageuka damu. Sehemu moja ya tatu ya viumbe vinavyoishi katika bahari vikakufa, na sehemu moja ya tatu ya mashua ikaharibika. Kisha malaika wa tatu akapiga baragumu. Halafu nyota kubwa iliyowaka kama mwenge, ikaanguka toka mbinguni na kujitupa juu ya sehemu moja ya tatu ya mito na juu ya chemichemi. (Jina la ile nyota ni Uchungu.) Basi sehemu moja ya tatu ya maji ikakuwa uchungu, na watu wengi waliokunywa maji yale walikufa kwa sababu ya sumu iliyokuwa ndani yake. Kisha malaika wa ine akapiga baragumu. Sehemu moja ya tatu ya jua ikaharibishwa pamoja na sehemu moja ya tatu ya mwezi na ya nyota. Sehemu zile tatu zikaingiwa na giza. Hivi hakukuwa mwangaza kwa muda wa sehemu moja ya tatu ya saa za muchana na sehemu moja ya tatu ya saa za usiku vilevile. Kisha nikaangalia tena, nami nikasikia tai mumoja akiruka juu sana katika anga akisema hivi kwa sauti kubwa: “Ole! Ole! Ole kwa wakaaji wa dunia, kutakaposikilika mulio wa zile baragumu zingine ambazo wamalaika watatu wanatayarisha kupiga!” Kisha malaika wa tano akapiga baragumu. Halafu nikaona nyota iliyokuwa imeshuka toka mbinguni, na kuanguka katika dunia. Nayo ikapewa ufunguo wa shimo ndefu la kuzimu. Nyota ile ikafungua hilo shimo. Moshi unaokuwa kama moshi wa furu kubwa ukapanda toka ndani ya shimo lile. Giza la ule moshi uliotoka ndani ya lile shimo ulifunika jua na anga. Nzige wakatokea katika ule moshi, na kusambaa juu ya dunia. Nao wakapewa nguvu zinazokuwa kama za nge. Wakaambiwa wasiharibu majani yoyote wala mumea wowote, wala muti wowote, lakini wawatese watu wasiokuwa na chapa ya muhuri wa Mungu kwenye paji za nyuso zao. Nzige wale hawakupewa amri ya kuwaua watu wale, lakini wawatese kwa muda wa miezi mitano. Na maumivu yao yalikuwa kama vile nge wakati anapouma mutu. Na kwa muda ule, watu watatafuta kifo, lakini hakitawapata. Watatamani kufa, lakini kifo kitawakimbia. Umbo la nzige wale lilifanana na farasi waliopambwa kwa kupigana vita. Juu ya vichwa vyao kulikuwa vitu vinavyofanana na taji za zahabu, na nyuso zao zilifanana kama nyuso za watu. Nywele zao zilikuwa sawa nywele za wanawake, na meno yao yalikuwa kama meno ya simba. Na juu ya vifua vyao kulikuwa vitu vinavyofanana na ngao za chuma. Na sauti ya mabawa yao ilikuwa kama uvumi wa magari yanayovutwa na farasi wengi wanaokimbia mbio kwenda kwa vita. Walikuwa na mikia kama ya nge na yenye kuchoma kama miiba. Uwezo wao wa kuwatesa watu kwa muda wa ile miezi mitano ulikuwa ndani ya mikia yao. Na mufalme wao, ndiye malaika wa lile shimo ndefu la kuzimu, jina lake liliitwa kwa Kiebrania “Abidani” na kwa kigriki “Apolioni” (maana yake “Mwangamizaji”). Hasara ya kwanza imepita, na nyuma ya ile kutatokea hasara zingine mbili. Malaika wa sita akapiga baragumu. Halafu nikasikia sauti moja ikitokea kwenye pembe ine za mazabahu ya zahabu iliyokuwa mbele ya Mungu. Sauti ile ikamwambia yule malaika wa sita aliyeshika baragumu hivi: “Uwafungue wale wamalaika wane waliofungwa kwenye muto mukubwa Furati.” Wale wamalaika wane wakafunguliwa, nao walikuwa wamewekwa tayari kwa saa ile, siku, mwezi na mwaka ule, wapate kuua sehemu moja ya tatu ya wanadamu. Nikasikia hesabu ya makundi ya waaskari wapanda-farasi, nao walikuwa milioni mia mbili. Na katika maono yale, nikaona wale farasi pamoja na wale waaskari waliopanda juu yao. Waaskari wale walikuwa na ngao zenye rangi nyekundu kama moto na zingine za rangi ya samawi na ya kimanjano kama kiberiti. Vichwa vya farasi wale vilikuwa kama vichwa vya simba, na ndani ya vinywa vyao mulitoka moto, moshi na mawe ya viberiti. Na sehemu moja ya tatu ya wanadamu wakauawa kwa mapigo hayo matatu: kwa moto, moshi na viberiti vilivyotoka ndani ya vinywa vya wale farasi, kwa maana uwezo wa wale farasi ulikuwa ndani ya vinywa vyao na ya mikia yao vilevile. Mikia yao ilikuwa kama kichwa cha nyoka, na kwa mikia hiyo waliweza kuzuru watu. Watu waliobaki bila kuuawa na yale mapigo hawakuachana na sanamu walizojitengenezea wao wenyewe. Hawakuacha kuabudu pepo, sanamu za zahabu, za feza, za shaba, za mawe na za miti zisizoweza kuona, wala kusikia, wala kutembea. Watu wale hawakuacha hata matendo yao ya uuaji, ya uchawi, ya uasherati na ya wizi. Kisha nikaona malaika mwingine mwenye uwezo akishuka toka mbinguni. Alikuwa akifunikwa na wingu, naye alikuwa na upindi wa mvua juu ya kichwa chake. Uso wake ulingaa kama jua na miguu yake ilimetameta kama nguzo ya ndimi za moto. Alikuwa akishika kitabu kidogo chenye kufunguliwa. Halafu akaweka muguu wake wa kuume juu ya bahari na muguu wa kushoto juu ya inchi kavu. Akalalamika kwa sauti kubwa kama simba anayenguruma. Na alipokwisha kulalamika, kukasikilika mulio wa ngurumo saba ya radi. Na ngurumo zile saba zilipokwisha kusikilika, nikajitayarisha kwa kuandika. Lakini nikasikia sauti kutoka mbinguni, ikiniambia hivi: “Uchunge kwa siri maneno yaliyosemwa na zile ngurumo saba.” Halafu yule malaika niliyemwona akisimama juu ya bahari na inchi kavu akainua mukono wake wa kuume juu. Akaapa kwa jina la Mungu anayeishi kwa milele na milele, muumba wa mbingu na vitu vyote vinavyokuwa ndani yake, nayo dunia na vyote vinavyokuwa ndani yake, pamoja na bahari na vitu vyote vinavyokuwa ndani yake, na kusema: “Hakutakuwa tena muda unaobaki!” Lakini wakati malaika wa saba atakapopiga baragumu, Mungu atatimiza mipango yake aliyoficha sawa vile alivyotangaza kwa kinywa cha manabii waliomutumikia. Kisha nikasikia tena sauti kutoka mbinguni ikiniambia: “Kwenda utwae kile kitabu kidogo chenye kufunguliwa katika mukono wa yule malaika anayesimama juu ya bahari na juu ya inchi kavu.” Nami nikaenda karibu na yule malaika, nikamwomba anipe kile kitabu kidogo. Naye akaniambia: “Ukitwae na ukikule, kitakuwa uchungu katika tumbo lako, lakini kitakuwa kitamu kama asali ndani ya kinywa chako.” Basi nikatwaa kitabu kile kidogo toka katika mukono wake, nikakikula. Kikakuwa kitamu kama asali ndani ya kinywa changu, lakini wakati nilipokimeza, nikasikia uchungu ndani ya tumbo langu. Kisha wakaniambia: “Imekupasa kutoa unabii tena kwa jamaa, kwa mataifa, kwa watu wa kila luga na kwa wafalme wengi.” Kisha wakanipa fimbo ya kupima urefu na kuniambia: “Simama upime hekalu la Mungu pamoja na mazabahu na kuwahesabu watu wanaoabudu ndani yake. Lakini uache kiwanja kinachokuwa inje ya hekalu, usikipime kwa maana kimetolewa kwa watu wa mataifa mengine watakaokanyaga muji mutakatifu kwa muda wa miezi makumi ine na miwili. Nami nitawatuma washuhuda wangu wawili, wakiwa wamevaa nguo za kilio. Nao watatangaza ujumbe wa Mungu kwa muda wa siku elfu moja mia mbili na makumi sita.” Wale washuhuda wawili ndiyo ile miti miwili ya mizeituni na vile vinara viwili vya kuwekea taa vinavyosimama mbele ya Bwana wa dunia. Na kama mutu akitaka kuwazuru, moto unatoka katika vinywa vyao na kuteketeza waadui zao. Ni vile ndivyo mutu anayetaka kuwazuru anavyopaswa kuuawa. Nao wako na uwezo wa kufunga mbingu kusudi mvua isinyeshe wakati wanapotangaza ujumbe wa Mungu. Wako vilevile na uwezo wa kugeuza maji kuwa damu, na uwezo wa kuleta mapigo ya kila namna kila wakati wanapotaka. Wakati watakapomaliza kutoa huo ushuhuda wa Mungu, yule nyama wa ajabu anayetoka katika kuzimu atapigana vita nao, naye atawashinda na kuwaua. Maiti zao zitabaki katika barabara ya muji ule mukubwa unaoitwa kwa fumbo Sodoma au Misri. Ni ndani ya muji ule Bwana wao alitundikwa juu ya musalaba. Nao watu wa kila jamaa, wa kila kabila, wa kila luga na wa kila taifa wataangalia maiti hizo kwa muda wa siku tatu na nusu, wala hawatakubali zizikwe. Wakaaji wa dunia watafurahi kwa ajili ya kifo chao na kushangilia. Watatumiana zawadi, kwa maana manabii hawa wawili waliwasumbua sana wakaaji wa dunia. Lakini nyuma ya zile siku tatu na nusu, pumzi ya uzima inayotoka kwa Mungu ikaingia ndani ya maiti zao, nao wakasimama. Na watu wote waliowaona wakashikwa na woga mukubwa. Manabii hao wawili wakasikia sauti kubwa toka mbinguni ikiwaambia: “Mupande huku!” Wakapanda mbinguni wakizungukwa na wingu, wale waadui zao wakiwa wakiwaangalia. Na saa ile ile, kukatokea tetemeko kubwa la inchi, na sehemu moja ya kumi ya muji ikabomoka, na watu elfu saba wakakufa katika tetemeko lile. Watu waliobaki wakashikwa na hofu, nao wakamutukuza Mungu wa mbinguni. Hasara ya pili imepita, na hasara ya tatu haitakawia kutokea! Kisha malaika wa saba akapiga baragumu. Halafu sauti kubwa zikasikilika katika mbingu, zikisema: “Sasa utawala juu ya dunia ni wa Bwana wetu na wa Masiya wake. Naye atatawala kwa milele na milele!” Na wale wazee makumi mbili na wane wanaokaa juu ya viti vyao vya kifalme mbele ya Mungu, wakainama uso mpaka chini wakimwabudu Mungu, wakisema: “Tunakushukuru wewe Bwana wetu, Mungu Mwenye Uwezo, unayekuwa na uliyekuwa, kwa maana umetumia uwezo wako mukubwa nawe ukasimika ufalme wako. Watu wa mataifa mengine walikasirika, lakini kasirani yako imetokea. Sasa ni wakati wa kuhukumu waliokufa, nao wakati wa kuwapa waliokutumikia zawadi, ndio manabii wako, na wote wanaoheshimu jina lako, wakubwa na wadogo. Ni wakati wa kuangamiza wale wanaoharibu dunia!” Kisha hekalu la Mungu linalokuwa mbinguni likafunguliwa, na Sanduku la Agano lake likaonekana ndani yake. Halafu kukatokea umeme, makelele, ngurumo ya radi, tetemeko la inchi na mvua kubwa ya mawe. Kisha kukaonekana kitambulisho kikubwa mbinguni. Kulikuwa mwanamuke aliyekuwa amefunikwa na jua, na mwezi chini kwenye miguu yake. Na juu ya kichwa kulikuwa taji lenye nyota kumi na mbili. Mwanamuke yule alikuwa mimba, naye alikuwa akilia kwa sababu ya uchungu na maumivu ya kuzaa. Kisha kukaonekana kitambulisho kingine mbinguni. Kulikuwa nyoka mukubwa mwekundu mwenye vichwa saba na pembe kumi. Juu ya kila kichwa kulikuwa taji saba. Mukia wake ulikokota sehemu moja ya tatu ya nyota za mbingu na kuzitupa katika dunia. Yule nyoka akasimama mbele ya yule mwanamuke aliyekuwa tayari kuzaa, kusudi amumeze mutoto wakati atakapozaliwa. Halafu yule mwanamuke akazaa mutoto mwanaume atakayetawala mataifa yote kwa fimbo ya chuma. Lakini mutoto yule akanyanyuliwa na kupelekwa kwa Mungu kwenye kiti chake cha kifalme. Na yule mwanamuke akakimbilia katika jangwa kwenye nafasi Mungu aliyomutayarishia kusudi apate kulishwa kule kwa muda wa siku elfu moja mia mbili makumi sita. Halafu kukatokea vita katika mbingu. Mikaeli na wamalaika zake wakapigana na yule nyoka mukubwa. Naye yule nyoka akapigana nao pamoja na wamalaika zake, lakini akashindwa na haikuwezekana tena kwake kukaa mbinguni pamoja na wamalaika zake. Basi yule nyoka mukubwa akafukuzwa. Yeye ndiye yule nyoka wa zamani anayeitwa “Mwovu” au “Shetani,” anayedanganya watu wote. Akatupwa katika dunia pamoja na wamalaika zake. Kisha nikasikia sauti kubwa kutoka mbinguni, ikisema: “Sasa wokovu, uwezo na ufalme wa Mungu, na mamlaka ya Kristo wake vimefika. Ni vile, kwa yule aliyekuwa akiwashitaki wandugu zetu mbele ya Mungu wetu muchana na usiku ametupwa chini ya mbingu. Wandugu zetu wamemushinda kwa nguvu ya damu ya Mwana-Kondoo na kwa njia ya ukweli walioshuhudia. Wao walikubali kutoa maisha yao mpaka kufa. Kwa sababu hii, ninyi munaokaa mbinguni, nayo mbingu kwa jumla, mushangilie! Ole kwenu ninyi munaokaa katika dunia na katika bahari kwa maana yule Mwovu ameshuka kwenu, naye anajaa na hasira, kwa sababu anajua kwamba wakati unaomubakilia ni mudogo.” Na wakati yule nyoka alipotambua kwamba ametupwa katika dunia, akaanza kumufuatilia yule mwanamuke aliyezaa mutoto mwanaume. Lakini yule mwanamuke akapewa mabawa mawili yanayokuwa kama ya tai, kusudi apate kuruka kwenda katika jangwa kwenye nafasi aliyotengenezewa, mbali na yule nyoka. Na kule apate kukulishwa kwa muda wa miaka mitatu na nusu. Basi yule nyoka akatokeza maji kwa uwingi ndani ya kinywa chake, nayo yakatelemuka kama muto nyuma ya yule mwanamuke kusudi yapate kumupeleka. Lakini udongo ukamusaidia yule mwanamuke; ukabomoka kama vile kinywa na kumeza ule muto uliotoka katika kinywa cha yule nyoka. Yule nyoka akamukasirikia yule mwanamuke na kwenda kufanya vita na wazao wake wengine; ndio wale wanaoshika amri za Mungu na kufuata ukweli ulioshuhudiwa na Yesu Kristo. Na yule nyoka akasimama kwenye kivuko cha bahari. Kisha nikaona nyama mumoja wa ajabu akitokea ndani ya bahari. Alikuwa na vichwa saba na pembe kumi. Na juu ya kila pembe lake kulikuwa taji, na juu ya vichwa vile kulikuwa kumeandikwa jina la kumutukana Mungu. Yule nyama niliyemwona alifanana na chui. Miguu yake ilikuwa kama ya dubu na kinywa chake kilikuwa kama kinywa cha simba. Yule nyoka mukubwa akamupa uwezo wake pamoja na kiti chake cha kifalme na mamlaka makubwa. Kimoja cha vichwa vya yule nyama kilionekana kwamba kilikuwa kimeumizwa vibaya sana, lakini kidonda kilichokuwa cha hatari ya kufa kilikuwa kimekwisha kupona. Na kwa hiyo watu wote wa dunia wakashangaa na kumufuata yule nyama. Nao wakaanza kumwabudu yule nyoka kwa sababu alimupa yule nyama uwezo wake. Vilevile wakamwabudu yule nyama, wakisema: “Ni nani anayefanana na nyama huyu? Ni nani anayeweza kupigana vita naye?” Yule nyama akapewa uwezo wa kusema maneno ya kiburi ya kumutukana Mungu. Naye akapewa mamlaka ya kufanya kazi yake kwa muda wa miezi makumi ine na miwili. Basi yule nyama akaanza kumutukana Mungu, akatukana jina lake na makao yake na wale wanaokaa mbinguni. Akapewa ruhusa ya kupigana vita na watu wa Mungu na kuwashinda. Akapewa hata mamlaka ya kutawala watu wote, wa kila kabila, kila jamaa, kila luga na kila taifa. Wakaaji wote wa dunia watamwabudu, ndio wale wote ambao tangia kuumbwa kwa dunia, majina yao hayakuandikwa katika kitabu cha uzima cha Mwana-Kondoo aliyechinjwa. “Mwenye kuwa na masikio, asikie. Mutu yule aliyekusudiwa kuwa mufungwa, atafungwa; na yule aliyekusudiwa kuuawa kwa upanga, atauawa kwa upanga. Kwa sababu hiyo, watu wa Mungu wanapaswa kuwa wavumilivu na wenye imani.” Kisha nikaona nyama wa pili wa ajabu akitokea ndani ya udongo. Alikuwa na pembe mbili zinazokuwa kama za mwana-kondoo naye alikuwa akisema kama nyoka mukubwa. Yeye alitumikisha mamlaka yote aliyopewa na yule nyama wa kwanza mbele yake. Alilazimisha vyote vinavyokuwa katika dunia pamoja na wakaaji wake kumwabudu yule nyama wa kwanza aliyekuwa na kovu la kidonda cha hatari. Yule nyama mukubwa wa pili alifanya kitambulisho kikubwa hata akashusha moto toka mbinguni mpaka juu ya dunia mbele ya watu wote. Akawadanganya wakaaji wa dunia kwa njia ya vitambulisho alivyowezeshwa kuonyesha mbele ya yule nyama mukubwa wa kwanza. Aliwaambia watu wa dunia watengeneze sanamu kwa heshima ya yule nyama aliyeumizwa kwa upanga, lakini aliendelea kuishi. Kisha yule nyama mukubwa wa pili akapewa uwezo wa kupuliza pumzi ya uzima ndani ya sanamu ya yule nyama mukubwa wa kwanza kusudi sanamu ile ipate kusema na kuweza kuua watu wasioiabudu. Na yule nyama akawalazimisha watu wote, wadogo na wakubwa, watajiri na wamasikini, wanaokuwa huru na watumwa, wapigwe chapa juu ya mikono yao ya kuume na juu ya paji za nyuso zao. Na hakukukuwa mutu aliyeweza kununua wala kuuzisha kitu pasipo kuwa na chapa ya jina la nyama yule au tarakimu zinazolingana na herufi za jina lile. Hapa inafaa kuwa na hekima. Yule anayekuwa na akili afafanue hesabu ya tarakimu zinazolingana na jina la yule nyama, kwa maana tarakimu ile ni ya mutu fulani. Nayo ni mia sita makumi sita na sita. Kisha nikaangalia, nikaona Mwana-Kondoo akisimama juu ya mulima Sayuni. Naye alikuwa pamoja na watu elfu mia moja makumi ine na ine, na juu ya paji za nyuso za watu wale kulikuwa kumeandikwa jina lake na jina la Baba yake. Nikasikia sauti kutoka mbinguni ikinguruma kama uvumi wa maporomoko ya maji mengi na kama ngurumo kubwa ya radi. Sauti ile ilisikilika kama vile sauti ya wapiga vinubi wakati wanapopiga vinubi vyao. Wale watu elfu mia moja makumi ine na ine waliimba wimbo mupya mbele ya kile kiti cha kifalme na mbele ya vile viumbe vine vya ajabu na ya wale wazee. Hakuna mutu aliyeweza kujifunza wimbo ule, isipokuwa wale watu elfu mia moja makumi ine na ine waliokombolewa katika dunia. Watu wale ndio waliojilinda katika usafi bila kujichafua kwa kulala na wanawake, nao wanamufuata Mwana-Kondoo kila fasi anapokwenda. Wamekombolewa kati ya watu wengine kusudi wakuwe wa kwanza kutolewa kwa Mungu na kwa Mwana-Kondoo kama vile sadaka ya mavuno ya kwanza. Wao hawakusema uongo hata mara moja; wako bila kosa. Kisha nikaona malaika mwingine akiruka juu sana katika mbingu akiwa na Habari Njema ya milele ya kupasha kwa wakaaji wa dunia, kwa watu wa kila taifa, wa kila kabila, wa kila luga na kila jamaa. Halafu akasema kwa sauti kubwa: “Mumuheshimu Mungu na kumutukuza, kwa sababu saa yake ya kuwahukumu watu imetimia. Mumwabudu yule aliyeumba mbingu na dunia, bahari na chemichemi za maji.” Malaika wa pili akafuata yule wa kwanza akisema: “Umebomoka, umebomoka kabisa, ule muji mukubwa Babeli. Umewakunywesha mataifa yote divai yake kali, ukiwalewesha na maovu ya uasherati wake.” Na malaika wa tatu akafuata wale wawili wa kwanza, akisema kwa sauti kubwa: “Kila mutu anayeabudu yule nyama na sanamu yake na kupigwa chapa juu ya paji la uso wake au juu ya mukono wake, naye vilevile atakunywa divai kali ya hasira ya Mungu iliyotengenezwa pasipo kuchangwa na maji na kumimiwa ndani ya kikombe chenye kujaa kasirani yake! Na watu kama wale, watateswa ndani ya moto na ndani ya mawe ya kiberiti yanayowaka moto mbele ya wamalaika watakatifu na mbele ya Mwana- Kondoo. Na moshi wa ule moto wa mateso yao utakuwa ukipanda juu kwa milele na milele. Wale walioabudu yule nyama na sanamu yake na mutu yeyote aliyepigwa chapa ya jina lake, hawatapumzika hata siku moja usiku na muchana.” Kwa sababu hiyo, watu wa Mungu wanaoshika amri za Mungu na kumwamini Yesu wanapaswa kuwa wavumilivu. Tena nikasikia sauti kutoka mbinguni, ikisema: “Andika maneno haya: ‘Heri tangu sasa kwa watu wanaokufa wakimwamini Bwana!’ ” Naye Roho anasema: “Ndiyo, ni kweli. Watapumzika toka katika masumbuko yao, kwa maana matendo yao yatafuatana nao.” Niliangalia tena, nami nikaona wingu jeupe, na juu ya wingu lile kulikuwa kukiikaa kiumbe kimoja kinachofanana na Mwana wa Mutu. Juu ya kichwa chake kulikuwa taji la zahabu, naye alikuwa akishika kisu kikali cha kuvuna katika mukono wake. Malaika mwingine akatoka katika hekalu, akalalamika kwa sauti kubwa akimwambia yule aliyeikaa juu ya wingu: “Nyoosha kisu chako, uanze kuvuna, kwa maana dunia iko tayari kwa kuvunwa, nayo saa ya mavuno imetimia!” Basi yule aliyeikaa juu ya wingu, akanyoosha kisu chake juu ya dunia na kuvuna dunia. Malaika mwingine akatoka katika hekalu linalokuwa mbinguni, akiwa na kisu kikali cha kuvuna. Kisha kukatokea malaika mwingine mwenye uwezo wa kuamuru moto, akatoka kwenye mazabahu, akamwambia kwa sauti kubwa yule aliyekuwa na kisu kikali cha kuvuna: “Nyoosha kisu chako, ukate matunda ya mizabibu yanayokuwa katika dunia kwa maana zabibu zimekomaa.” Yule malaika akanyoosha kisu chake juu ya dunia, akachuma mizabibu ya dunia, akaitupa katika kikamulio kikubwa cha zabibu chenye kujaa kasirani ya Mungu. Zile zabibu zikakamuliwa mbali na muji, damu ikatiririka toka ndani ya kile kikamulio mpaka ikafika kwenye umbali wa kilometre yapata mia tatu. Nao urefu kwenda chini wa ile damu ulikuwa yapata metre moja na nusu. Kisha nikaona tena katika mbingu kitambulisho kingine kikubwa na cha kushangaza sana. Kulikuwa wamalaika saba wanaoshika mapigo saba. Mapigo haya ndiyo yaliyokuwa ya mwisho, kwa maana ni yale Mungu atakayotumia kwa kutimiza kasirani yake. Tena nikaona kitu kinachofanana na bahari ya kioo, iliyochanganyika na moto. Nikaona vilevile wale walioshinda yule nyama wa ajabu pamoja na sanamu yake na tarakimu zinazolingana na herufi za jina lake. Watu wale walikuwa wakisimama juu ya ile bahari ya kioo wakishika vinubi walivyopewa na Mungu. Waliimba wimbo wa Musa, mutumishi wa Mungu, na wimbo wa Mwana- Kondoo wakisema: “Ewe Bwana wetu, Mungu Mwenye Uwezo, matendo yako ni makubwa na ya ajabu! Ewe Mufalme wa mataifa, kazi zako ni za haki na za kweli! Ewe Bwana, hakuna asiyekuogopa, wala hakuna asiyekutukuza, kwa maana wewe peke yako ndiwe mutakatifu. Mataifa yote yatakuja kukuabudu, kwa maana matendo yako ya haki yameonyeshwa wazi.” Na nyuma ya pale nikaona hekalu limefunguliwa mbinguni; mule mulikuwa hema yenye vibao vya agano la Mungu. Na wale wamalaika saba walioshika mapigo saba wakatoka katika lile hekalu. Walikuwa wamevaa nguo zilizofumwa na nyuzi za pamba zenye kungaa na mikaba ya zahabu katika viuno vyao. Na mumoja wa vile viumbe vine vya ajabu akawapa wale wamalaika saba vikombe saba vya zahabu vyenye kujaa kasirani ya Mungu, anayeishi kwa milele. Hekalu likajaa moshi kutokana na utukufu wa Mungu na uwezo wake. Na hakuna mutu aliyeweza kuingia ndani ya hekalu mpaka yale mapigo yaliyoletwa na wale wamalaika saba yalipotimizwa. Kisha nikasikia sauti kubwa ikitoka katika hekalu ikiwaambia wale wamalaika saba: “Mwende kumwanga vile vikombe saba vya kasirani ya Mungu juu ya dunia!” Malaika wa kwanza akamwanga kikombe chake katika dunia. Halafu majipu mabaya na yenye kuumiza sana yakaota juu ya watu waliokuwa na chapa ya yule nyama na walioabudu sanamu yake. Malaika wa pili akamwanga kikombe chake katika bahari. Maji yakageuka na kuwa kama damu ya mufu, na viumbe vyote vyenye uzima vilivyokuwa ndani ya bahari vikakufa. Malaika wa tatu akamwanga kikombe chake katika mito na chemichemi za maji, na maji yao yakageuka damu. Nikasikia malaika anayekuwa na uwezo wa kuamuru maji akisema: “Ewe Mutakatifu unayekuwa na uliyekuwa, wewe unahukumu kufuatana na haki. Watu hawa walimwanga damu ya watu wako na ya manabii wako, kwa sababu hiyo sasa umewakunywesha damu, nao wanastahili kutendewa vile!” Kisha nikasikia sauti ikitoka kwenye mazabahu, ikisema: “Hakika, ewe Bwana wetu, Mungu Mwenye Uwezo, wewe unatoa hukumu za kweli na za haki!” Malaika wa ine akamwanga kikombe chake juu ya jua, nalo likapewa uwezo wa kuwaunguza watu kwa joto lake. Watu wakaunguzwa na lile joto kali, hata wakatukana jina la Mungu anayekuwa na uwezo wa kuamuru mapigo yale. Wakakataa kugeuka toka zambi zao na kumutukuza Mungu. Malaika wa tano akamwanga kikombe chake juu ya kiti cha kifalme cha yule nyama wa ajabu, na ufalme wake ukafunikwa na giza. Watu wakaanza kutafuna ndimi zao kwa sababu ya maumivu. Wakamutukana Mungu wa mbinguni kwa sababu ya maumivu yao na yale majipu yao, lakini hawakuacha matendo yao mabaya. Malaika wa sita akamwanga kikombe chake katika muto mukubwa Furati. Maji yake yakakauka kusudi njia itengenezwe kwa ajili ya wafalme wanaotoka mashariki. Halafu nikaona pepo wachafu watatu wanaofanana na vyura wakitoka ndani ya kinywa cha yule nyoka mukubwa, na ndani ya kinywa cha yule nyama wa ajabu na cha yule nabii wa uongo. Hawa ndio pepo wanaoonyesha vitambulisho. Nao ndio wanaokwenda kwa wafalme wote wa dunia na kuwakusanya kwa kupigana vita Siku ile kubwa ya Mungu Mwenye Uwezo. “Sikiliza, ninakuja kwa saa isiyozaniwa kama vile mwizi. Heri yule anayekesha na kutunza nguo zake vizuri kusudi asitembee uchi na kujifezehesha mbele ya watu.” Na wale pepo wakawakusanya wale wafalme kwenye nafasi inayoitwa katika Kiebrania “Harmagedoni.” Malaika wa saba akamwanga kikombe chake katika anga. Halafu sauti kubwa ikasikilika kutoka katika hekalu kwenye kiti cha kifalme ikisema: “Sasa ni mwisho!” Kukatokea umeme, makelele, ngurumo ya radi na tetemeko kubwa la inchi lisilotokea bado tangia watu walipoanza kuishi katika dunia. Kweli tetemeko lile lilikuwa kubwa sana! Na ule muji mukubwa ukagawanyika katika sehemu tatu, na miji ya mataifa yote ikabomoka. Mungu hakusahau muji mukubwa Babeli, akaukunywesha kikombe kinachokuwa na divai ya kasirani yake kali. Visanga vyote vikatoweka na milima haikuonekana tena. Kisha mvua ya mawe makubwa yenye uzito wa zaidi ya kilo makumi ine ikanyesha juu ya watu. Nao wakamutukana Mungu kwa sababu ya hilo pigo la mvua ya mawe, kwa maana pigo lile lilileta hasara kubwa sana. Halafu mumoja wa wale wamalaika saba walioshika vile vikombe saba akajongea na kuniambia: “Kuja nitakuonyesha namna gani yule kahaba mukubwa atakavyohukumiwa, ndio ule muji uliojengwa katikati ya mito mingi. Wafalme wa dunia wamefanya uzinzi pamoja naye, na wakaaji wa dunia wamelewa divai ya uasherati wake.” Nikashikwa na Roho wa Mungu, na malaika akanipeleka katika jangwa. Kule nikaona mwanamuke aliyekuwa akiikaa juu ya nyama mumoja wa ajabu mwekundu aliyeandikwa juu yake majina ya kumutukana Mungu. Nyama yule alikuwa na vichwa saba na pembe kumi. Yule mwanamuke alikuwa amevaa nguo za rangi nyekundunyeusi na nyekundu sana za bei kali, tena alikuwa amejipamba kwa zahabu, mawe ya bei kali na ushanga wa bei kali. Naye alikuwa anashika katika mukono wake kikombe kilichotengenezwa na zahabu chenye kujaa machukizo na mambo machafu ya uasherati wake. Alikuwa ameandikwa juu ya paji la uso wake jina lenye fumbo: “Muji mukubwa Babeli, mama ya washerati na machukizo ya dunia.” Nikaona kwamba yule mwanamuke amelewa kwa damu ya watu wa Mungu na ya watu waliouawa kwa sababu ya ushuhuda wao kwa ajili ya Yesu. Wakati nilipomwona nikashangaa sana. Halafu yule malaika akaniuliza: “Kwa nini unashangaa? Nitakuambia maana ya fumbo la mwanamuke yule na ya yule nyama anayemubeba, na anayekuwa na vichwa saba na pembe kumi. Yule nyama uliyemwona alikuwa yuko zamani, lakini sasa hayuko tena. Naye ni tayari kupanda toka katika shimo la kuzimu na kwenda kuangamizwa kabisa. Nao wakaaji wa dunia ambao majina yao hayakupata kuandikwa katika kitabu cha uzima tangia kuumbwa kwa dunia, watashangaa wakati watakapomwona yule nyama, kwa sababu alikuwa yuko zamani lakini hayuko sasa, naye atatokea tena! “Hapa inafaa kuwa na akili na hekima. Vile vichwa saba ni milima saba, ambavyo yule mwanamuke anaikaa juu yake. Vile vichwa ni vilevile wafalme saba. Watano kati yao wamekwisha kuangushwa chini, mumoja angali anatawala na mwingine hajafika bado; naye atakapofika, atabaki kwa muda mufupi tu. Yule nyama aliyekuwa yuko zamani, lakini sasa hayuko tena, yeye mwenyewe ni mufalme wa nane, ni mumoja wa wale saba naye anakwenda kuangamia kabisa. “Zile pembe kumi ulizoona ni wafalme kumi, ambao hawajaanza bado kutawala, lakini watapewa mamlaka ya kutawala kama wafalme kwa muda wa saa moja pamoja na yule nyama. Hawa wote kumi wako na shabaha moja ya kumupa yule nyama uwezo wao na mamlaka yao. Watapigana vita na Mwana-Kondoo, lakini Mwana-Kondoo pamoja na waaminifu wake aliowaita na kujichagulia atawashinda, kwa sababu yeye ni Bwana wa wabwana na Mufalme wa wafalme.” Yule malaika akaniambia tena: “Yale maji uliyoona pale yule kahaba anapoikaa, ni watu wa kila taifa, kila jamaa na kila luga. Zile pembe kumi ulizoona na yule nyama wa ajabu watamuchukia yule kahaba. Watamunyanganya vyote anavyokuwa navyo na kumwacha uchi. Nao watakula nyama ya mwili wake na kuteketeza mabaki yake kwa moto. Kwa maana Mungu ametia ndani yao nia ya kuwasukuma kutimiza shabaha yake nao wapate kufikia shauri moja na kumupa yule nyama madaraka yao ya kifalme mpaka maneno ya Mungu yatimie. Yule mwanamuke uliyemwona, ni ule muji mukubwa unaotawala wafalme wa dunia.” Kisha mambo hayo, nikaona malaika mwingine akishuka kutoka mbinguni. Yeye alikuwa na uwezo mukubwa; na dunia yote ilingaa kwa utukufu wake. Halafu akalalamika kwa sauti kubwa, akisema: “Umebomoka, umebomoka kabisa ule muji mukubwa Babeli! Sasa umekuwa makao ya mashetani ya kila namna, ya pepo wachafu, na makimbilio ya ndege wote wachafu na wenye kuchukiza. Ni kwa sababu mataifa yote yalileweshwa na divai kali ya uasherati wa muji ule. Wafalme wa dunia wamezini nao, na wachuuzi wa dunia wamejitajirisha kutokana na uwingi wa mali zake.” Kisha nikasikia sauti ingine kutoka mbinguni ikisema: “Mutoke katika muji ule ninyi watu wangu, kusudi musishiriki zambi zake na kupatwa vilevile na mapigo yatakayoupata. Kwa maana zambi zake zinazidi sana hata zimefika mbinguni na Mungu hakusahau mabaya yake. Mutendee muji ule sawa vile ulivyowatendea. Mulipize matendo yake mara mbili zaidi. Na katika kile kikombe alimochanganya divai yake, mumuchangie divai inayokuwa kali mara mbili zaidi kuliko ile aliyowapa. Na kwa kadiri ulivyojitukuza na kuishi katika raha, kwa kadiri ile ile muuletee mateso na huzuni. Muji ule unajisemesha: ‘Mimi ninaikaa juu ya kiti cha kifalme kama vile malkia; mimi si mujane, wala sitapata huzuni hata kidogo!’ Kwa sababu hiyo, kwa muda wa siku moja tu utapatwa na mapigo ya mauti, huzuni na njaa. Na zaidi ya hiyo utateketezwa kwa moto, kwa maana Bwana wetu, Mungu anayeuhukumu, ni mwenye uwezo.” Wafalme wa dunia waliozini nao na kujifurahisha pamoja nao wataulilia na kuufanyia kilio wakati watakapoona moshi wa moto utakaouteketeza ukipanda juu. Watasimama kwa mbali kwa ajili ya kuogopa yale mateso yake, wakisema: “Ole, ole kwako ewe muji Babeli, muji mukubwa na wenye uwezo! Kwa saa moja tu azabu yako imetimia!” Wachuuzi wa dunia watalia na kuufanyia kilio kwa sababu hakuna mutu atakayewanunulia tena biashara zao za zahabu, feza, mawe ya bei kali, ushanga, nguo zilizofumwa na nyuzi zuri pamoja na nguo nzuri za rangi nyekundu nyeusi na nyekundu sana, miti yote yenye kunuka vizuri, vyombo vyote vyenye kutengenezwa na pembe, na vyote vinavyochongwa na miti ya bei kali, na vyombo vyote vya shaba, vya chuma, vya mawe yenye kuchongwa, mudalasini, vitu vyote vya kufukiza, marasi, ubani, divai, mafuta, unga nzuri, ngano, ngombe, kondoo, farasi, magari, watumwa na hata roho za watu. Nao wale wachuuzi wanauambia muji ule: “Mazao mbalimbali uliyotamani sana kupata, yametoweka kwako. Na vitu vyote vya bei kali na vizuri vyenye kungaa vimekupotea, wala hautaviona tena.” Wachuuzi waliojitajirisha na biashara za muji ule, watasimama kwa mbali kwa ajili ya woga kwa kuona mateso yatakayoupata. Watalia na kufanya kilio, wakisema: “Ole! Ole kwa muji ule mukubwa. Ulikuwa unavaa nguo zilizofumwa na nyuzi nzuri pamoja na nguo zuri ya rangi nyekundu nyeusi na nyekundu sana. Ulikuwa unapambwa kwa zahabu, mawe ya bei kali, na ushanga wa bei kali! Kwa muda wa saa moja tu utajiri mwingi kama huu umeharibishwa.” Waongozi wote wa mashua na wasafiri wao, nao wote wanaofanya kazi ndani ya mashua na wote wanaochuuza kwa njia ya bahari walisimama kwa mbali. Walilalamika walipoona moshi wa moto uliouteketeza ukipanda juu wakisema: “Muji gani ungeweza kulinganishwa na muji huu mukubwa!” Wakajitupia mavumbi juu ya vichwa vyao, wakalia na kufanya kilio, nao walilalamika, wakisema: “Ole! Ole kwa muji ule mukubwa! Wote wanaokuwa na mashua za kufanya uchuuzi juu ya bahari walijitajirisha na mali zake nyingi. Lakini kwa muda wa saa moja tu umebaki mutupu.” Enyi mbingu, nanyi watu wa Mungu pamoja na mitume na manabii wake, mufurahi kwa ajili ya mambo yaliyotokea muji ule, kwa maana Mungu amewapatia haki yenu kwa kuuhukumu! Kisha malaika mumoja mwenye uwezo akanyanyua jiwe linalokuwa kama jiwe kubwa la kusagia. Akalitupa katika bahari akisema: “Ni hivi muji mukubwa wa Babeli utakavyotupwa kwa nguvu, nao hautaonekana tena. Sauti ya wapiga vinubi na ya wapiga vinanda, ya wapiga filimbi na ya baragumu, haitasikilika ndani yako tena. Fundi wa kazi yoyote hataonekana ndani yako tena hata kidogo wala kelele la jiwe la kusagia halitasikilika. Mwangaza wa taa hautaonekana tena ndani yako. Na hakutasikilika tena kelele la wenye kuoa au kuolewa. Itakutokea vile kwa sababu wachuuzi wako walikuwa wenye uwezo mukubwa katika dunia, nawe umewadanganya watu wote kwa njia ya vitendo vyako vya uchawi.” Muji Babeli umeazibiwa kwa sababu ndani yake kumeonekana damu ya manabii na ya watu wa Mungu pamoja na damu ya watu wote waliouawa katika dunia. Kisha mambo hayo, nikasikia kelele kutoka mbinguni linalosikilika kama vile sauti kubwa ya kundi kubwa la watu ikisema: “Mungu asifiwe! Wokovu, utukufu na uwezo ni vya Mungu wetu. Yeye anastahili utukufu na uwezo. Hukumu zake ni za kweli na za haki. Amehukumu yule kahaba mukubwa ambaye alikuwa akipotosha dunia kwa vitendo vyake vya uasherati. Mungu amemulipiza kisasi cha damu ya watumishi wake!” Nao wakasema tena: “Mungu asifiwe! Moshi wa moto unaoteketeza ule muji mukubwa unapanda juu kwa milele na milele!” Na wale wazee makumi mbili na wane na vile viumbe vine vya ajabu wakainama chini na kumwabudu Mungu, anayeikaa juu ya kiti cha kifalme, wakisema: “Amina! Mungu asifiwe!” Kisha sauti ikasikilika toka kwenye kiti cha kifalme ikasema: “Mumusifu Mungu wetu ninyi watumishi wake wote, ninyi wote munaomuheshimu, wakubwa na wadogo!” Kisha nikasikia sauti inayosikilika kama kelele la kundi kubwa la watu, na kama ngurumo ya maporomoko ya maji mengi na kama ngurumo kubwa ya radi ikisema: “Mungu asifiwe! Kwa maana yeye Bwana wetu, Mungu wetu Mwenye Uwezo anatawala. Tufurahi na kushangilia na kumutukuza, kwa sababu saa ya ndoa ya Mwana-Kondoo imetimia, naye bibi arusi wake amejitayarisha.” Yule bibi amepewa nguo ya kuvaa iliyofumwa na nyuzi nzuri zenye kungaa. (Nguo ile ni mufano wa matendo ya haki ya watu wa Mungu.) Halafu malaika akaniambia: “Andika maneno haya: Heri wale wanaoalikwa kwa karamu ya ndoa ya Mwana-Kondoo.” Naye akasema tena: “Maneno haya ni ya kweli yanayotoka kwa Mungu.” Nikaanguka mbele yake kusudi nimwabudu, lakini akaniambia: “Angalia, usifanye vile! Kwa maana mimi ni mutumishi kama vile wewe na wandugu zako wanaoshika ukweli ulioshuhudiwa na Yesu. Ni Mungu ndiye unayepaswa kumwabudu! Maana ukweli ambao Yesu alishuhudia, ndio uwezo unaowaongoza manabii.” Kisha nikaona mbingu imefunguka na kukatokea farasi mweupe. Yule aliyepanda juu yake anaitwa Mwaminifu na Mwenye Ukweli, kwa maana anahukumu na kupigana vita kwa haki. Macho yake yalimetameta kama ndimi za moto, na juu ya kichwa chake kulikuwa taji nyingi. Alikuwa na jina lililoandikwa juu yake, wala hakuna mutu aliyejua, isipokuwa yeye mwenyewe tu. Alikuwa amevaa nguo iliyochovywa ndani ya damu. Jina lake ni: “Neno la Mungu.” Makundi ya wakaaji wa mbinguni wakamufuata, nao walikuwa wakipanda juu ya farasi weupe na kuvaa nguo safi nyeupe za kitani. Ndani ya kinywa chake mulitoka upanga mukali kwa kushinda mataifa. Naye atatawala kwa fimbo ya chuma na kukamua zabibu ndani ya kikamulio cha divai kinachojaa kasirani kali ya Mungu Mwenye Uwezo. Na juu ya nguo yake na paja la muguu wake kulikuwa kumeandikwa jina hili: “Mufalme wa wafalme na Bwana wa wabwana.” Kisha nikaona malaika mumoja amesimama katika jua. Alikuwa akilalamikia ndege wote waliokuwa wakiruka juu katika anga akiwaambia: “Mukuje mukutane pamoja kwa karamu kubwa ya Mungu! Hivi mutakula nyama za miili ya wafalme, za majemadari, za watu wenye uwezo, nyama za farasi pamoja na za watu wanaopanda juu yao na nyama za watu wote wanaokuwa huru na za watumwa, wakubwa kama vile wadogo.” Nikaona yule nyama wa ajabu pamoja na wafalme wa dunia na makundi yao ya waaskari wamekusanyika pamoja kupigana vita na yule anayepanda juu ya farasi na kundi la waaskari wake. Yule nyama akakamatwa pamoja na yule nabii wa uongo aliyeonyesha vitambulisho mbele yake. (Ni kwa njia ya vitambulisho vile aliwadanganya wale waliopigwa chapa ya yule nyama na wale walioabudu sanamu yake.) Nyama yule pamoja na nabii wa uongo wakatupwa wangali wazima katika ziwa la moto munamowaka mawe ya kiberiti. Na wale waliobaki wakauawa kwa upanga uliotoka katika kinywa cha yule aliyepanda juu ya yule farasi. Ndege wote wakashibishwa na kula nyama za miili yao. Kisha nikaona malaika mumoja akishuka toka mbinguni. Yeye alikuwa akishika katika mukono wake ufunguo wa shimo ndefu la kuzimu na munyororo mukubwa. Akamukamata yule nyoka mukubwa, ndiye yule nyoka wa zamani, anayeitwa “Mwovu” au “Shetani” na kumufunga kwa muda wa miaka elfu moja. Malaika yule akamutupa ndani ya shimo ndefu la kuzimu. Akalifunga na kutia kitambulisho cha muhuri juu yake kwamba lisifunguliwe kusudi nyoka yule asiyadanganye tena mataifa mpaka ile miaka elfu moja ipate kutimia. Kisha miaka hiyo, anapaswa kufunguliwa tena kwa muda mufupi. Kisha nikaona viti vya kifalme na watu waliokuwa wakiikaa juu yao, wakapewa uwezo wa kuhukumu. Nikaona vilevile roho za wale waliochinjwa kwa sababu ya kutangaza ukweli ulioshuhudiwa na Yesu na Neno la Mungu. Watu wale hawakumwabudu yule nyama wa ajabu, wala sanamu yake, wala hawakupigwa chapa yake juu ya paji za nyuso zao, au juu ya mikono yao. Nao wakafufuka na kutawala pamoja na Kristo muda wa miaka elfu moja. (Wafu wengine waliobaki, hawakufufuka mpaka ile miaka elfu moja ipate kutimia.) Huu ndio ufufuko wa kwanza. Heri na baraka sana kwa wale watakaokuwa katika ufufuko wa kwanza! Kifo cha pili hakina uwezo juu yao, nao watakuwa makuhani wa Mungu na wa Kristo, na watatawala pamoja naye kwa muda wa miaka elfu moja. Wakati ile miaka elfu moja itakapotimia, Shetani atafunguliwa toka katika kifungo chake, naye atakwenda kuwadanganya watu wa mataifa wanaokuwa katika pande zote za dunia, ndio wanaoitwa Gogi na Magogi. Shetani atawakusanya kwa kupigana vita, nao watakuwa wengi kama vile muchanga wa bahari. Walitawanyika katika dunia yote, na kuzunguka kambi ya watu wa Mungu na muji wake alioupenda. Lakini moto ukashuka toka mbinguni, ukawateketeza. Kisha yule Mwovu aliyewadanganya, akatupwa katika ziwa la moto na lenye mawe ya kiberiti yanayowaka moto, pahali yule nyama wa ajabu na yule nabii wa uongo wanapokuwa. Nao watateswa muchana na usiku, milele na milele. Kisha nikaona kiti kikubwa cheupe cha kifalme pamoja na yule aliyeikaa juu yake. Dunia na mbingu vikatoweka mbele yake navyo havikuonekana tena. Nikaona wale waliokufa, wakubwa na wadogo wakisimama mbele ya kile kiti cha kifalme. Vitabu vikafunguliwa na kitabu kingine kikafunguliwa ndicho kitabu cha uzima. Wale waliokufa wakahukumiwa kufuatana na matendo yao sawa vile ilivyoandikwa katika vitabu. Bahari ikawarudisha wafu waliozama ndani yake. Kifo na kuzimu zikarudisha wafu waliokuwa ndani yao. Na kila mumoja akahukumiwa kufuatana na matendo yake. Kisha kifo na kuzimu vikatupwa katika ziwa la moto. Ziwa lile la moto ndicho kifo cha pili. Na mutu yeyote ambaye jina lake lililokosa kuandikwa katika kitabu cha uzima, alitupwa katika ziwa la moto. Kisha nikaona mbingu mupya na dunia mupya. Kwa sababu mbingu ya kwanza na dunia ya kwanza vilikuwa vimekwisha kutoweka, bahari nayo haikukuwa tena. Nikaona muji mutakatifu, ndio Yerusalema mupya, uliokuwa ukishuka toka mbinguni kwa Mungu, nao ukitengenezwa vizuri kama vile bibi arusi aliyepambwa kwa ajili ya kwenda kukutana na mume wake. Nikasikia sauti kubwa tokea kwenye kiti cha kifalme ikisema: “Sasa makao ya Mungu yanapatikana kati ya watu! Yeye atakaa pamoja nao, nao watakuwa watu wake. Mungu mwenyewe atakuwa pamoja nao, naye atakuwa Mungu wao. Yeye atapanguza machozi yao yote na kifo hakitakuwa tena, wala kilio, wala malalamiko, wala maumivu. Kwa maana dunia ya mbele imekwisha kupita.” Basi yule aliyekuwa akiikaa juu ya kiti cha kifalme akasema: “Angalia ninafanya vitu vyote kuwa vipya.” Kisha akaniambia: “Andika maneno haya, kwa maana ni ya kweli na ya uhakika.” Akasema tena: “Sasa ni mwisho! Mimi ni Alfa na Omega, mwanzo na mwisho. Yule anayesikia kiu, nitamupa maji ya kunywa yanayotoka katika chemichemi ya maji ya uzima pasipo kulipa. Yule atakayeshinda atapokea toka kwangu zawadi ile, mimi nitakuwa Mungu wake, naye atakuwa mwana wangu. Lakini watu wenye woga, wasioamini, wenye machukizo, wauaji, wazinzi, wachawi, wanaoabudu sanamu na wote wanaosema uongo, fungu lao ni katika lile ziwa la moto na ndani ya mawe ya kiberiti yanayowaka moto. Hiki ndicho kifo cha pili.” Kisha mumoja wa wale wamalaika saba walioshika vile vikombe vilivyojaa mapigo saba ya mwisho, akajongea na kuniambia: “Kuja nitakuonyesha bibi arusi, muke wa Mwana-Kondoo.” Nikashikwa na Roho, na malaika akanipeleka juu ya mulima mukubwa na murefu. Akanionyesha muji mutakatifu, ndio Yerusalema uliokuwa ukishuka toka mbinguni kwa Mungu, nao ukingaa kwa utukufu wa Mungu. Mwangaza wake ulikuwa kama jiwe la bei kali la yaspi, linalongaa kama kioo. Ulikuwa ukizungukwa na ukuta mukubwa na murefu wenye milango kumi na miwili na wamalaika kumi na wawili walichunga milango ile. Na juu ya milango ile, kulikuwa kumeandikwa majina ya makabila kumi na mawili ya Waisraeli. Kila upande kulikuwa milango mitatu: upande wa mashariki milango mitatu, upande wa kaskazini milango mitatu, upande kusini milango mitatu na upande wa magaribi milango mitatu. Na ukuta uliozunguka muji ule ulikuwa umejengwa juu ya mawe ya musingi kumi na mawili na juu ya kila jiwe kulikuwa kumeandikwa jina la kila mumoja wa mitume kumi na wawili wa Mwana-Kondoo. Malaika yule aliyekuwa akisema nami alikuwa na fimbo ya kupima ya zahabu kusudi apate kupima muji ule, milango yake na ukuta unaouzunguka. Muji ule ulikuwa umejengwa namna ya muraba, urefu wake na upana wake vilikuwa sawasawa. Malaika akapima muji ule na ile fimbo; ulikuwa na urefu, upana na urefu wake wa kwenda juu yapata kilometre elfu mbili na mia ine. Malaika akapima vilevile ukuta; ulikuwa yapata metre makumi sita kufuatana na kipimo cha kawaida cha wanadamu ambacho yule malaika alichotumia. Ukuta ulikuwa umejengwa na mawe ya bei kali ya yaspi, na muji wenyewe ulikuwa umejengwa na zahabu safi inayongaa kama kioo. Musingi wa ukuta uliozunguka muji ule ulikuwa unapambwa na mawe ya bei kali ya kila aina. Mawe ya musingi wa kwanza ulikuwa wa mawe ya yaspi, wa pili wa mawe ya safilo, wa tatu wa mawe ya kaledoni, wa ine wa mawe ya zumaridi, wa tano wa mawe ya sadoniki, wa sita wa mawe ya akiki, wa saba wa mawe ya krisolite, wa nane wa mawe ya belulo, wa tisa wa mawe ya topazo, wa kumi wa mawe ya krisoparazo, wa kumi na moja wa mawe ya haikinto na wa kumi na mbili wa mawe ya amazito. Na ile milango kumi na miwili ilikuwa ushanga nzuri kumi na mbili; kila mulango ulikuwa umetengenezwa na ushanga moja. Barabara ya muji ule ilikuwa imetengenezwa na zahabu safi inayongaa kama kioo. Sikuona hekalu ndani ya muji ule, maana Bwana wetu Mungu Mwenye Uwezo na yule Mwana-Kondoo ndio hekalu lake. Muji ule hauna lazima ya mwangaza wa jua, wala wa mwezi, kwa sababu utukufu wa Mungu unauangazia na Mwana-Kondoo ndiye taa yake. Kwa hiyo watu wa mataifa watatembea katika mwangaza wake na wafalme wa dunia wataleta utajiri wao ndani yake. Milango ya muji ule haitafungwa muchana maana ndani yake hakutakuwa usiku. Heshima na utukufu za watu wote wa mataifa zitaletwa ndani ya muji ule. Hakuna kitu chochote kichafu kitakachoingia ndani yake, wala yeye anayefanya machukizo na kusema uongo; lakini wale tu ambao majina yao yaliandikwa katika kitabu cha uzima cha Mwana-Kondoo. Kisha yule malaika akanionyesha muto wa maji ya uzima wenye kungaa kama kioo, uliokuwa ukitiririka toka kwenye kiti cha kifalme cha Mungu na cha Mwana-Kondoo. Muto ule ulitelemuka katikati ya barabara ya muji mutakatifu. Kandokando ya ule muto, kulikuwa kumeota muti wa uzima, nao unatoa matunda mara kumi na mbili kwa mwaka, maana yake mara moja kila mwezi. Majani ya muti ule yanatumiwa kama dawa ya kuponyesha mataifa. Hakutakuwa tena kitu chochote kinacholaaniwa na Mungu. Kiti cha kifalme cha Mungu na cha Mwana-Kondoo kitakuwa ndani ya muji ule, na watumishi wa Mungu watamwabudu. Wataona uso wake na jina lake litaandikwa juu ya paji za nyuso zao. Hakutakuwa usiku tena, wala hawatakuwa na lazima ya mwangaza wa taa wala jua, kwa sababu Bwana wetu na Mungu wetu mwenyewe atawaangazia, nao watatawala milele na milele. Kisha yule malaika akaniambia: “Maneno haya ni ya kweli na ya uhakika. Na Bwana Mungu anayewaongoza manabii kwa njia ya Roho wake ametuma malaika wake kwa kuwaonyesha watumishi wake mambo yanayopaswa kutokea kisha kidogo.” Yesu anasema: “Sikiliza, ninakuja upesi! Heri yule anayeshika maneno ya unabii yanayoandikwa katika kitabu hiki!” Ni mimi Yoane niliyesikia na kuona mambo hayo. Na wakati nilipokwisha kuyasikia na kuyaona, nilianguka mbele ya malaika aliyeyaonyesha kwangu kwa kumwabudu. Lakini akaniambia: “Angalia, usifanye vile! Kwa maana mimi ni mutumishi kama vile wewe, na wandugu zako manabii na watu wanaoshika maneno ya unabii yanayoandikwa katika kitabu hiki. Ni Mungu ndiye unayepaswa kumwabudu!” Kisha akaniambia: “Usichunge kwa siri maneno haya ya unabii wa kitabu hiki, kwa sababu wakati wa kutimia kwa mambo haya unakaribia. Mutu mubaya aendelee kufanya ubaya, na mutu muchafu azidi kuwa muchafu, na mutu mwema aendelee kutenda mema na mutu mutakatifu aendelee kuwa mutakatifu.” Yesu anasema: “Sikiliza, ninakuja upesi! Nitaleta mushahara kwa kulipa kila mumoja wenu kwa kadiri ya matendo yake. Mimi ni Alfa na Omega, mwanzo na mwisho.” Heri wale wanaosafisha kanzu zao, kwa maana watakuwa na haki ya kukula matunda ya muti wa uzima na ya kuingia katika muji ule kwa kupitia kwenye milango. Lakini mbali ya muji ule kuna watu wenye kuchukiza, wachawi, wazinzi, wauaji, wanaobudu sanamu na wasema uongo na wote wanaoupenda. “Mimi Yesu, nimemutuma malaika wangu kwa kuwashuhudia maneno haya yote katika kanisa. Mimi ni wa shina na wa uzao wa mufalme Daudi. Mimi ni nyota ya asubui.” Roho na Bibi arusi wanasema: “Kuja!” Naye mwenye kusikia maneno haya aseme vilevile: “Kuja!” Yule anayesikia kiu akuje, na yule anayetaka maji ya uzima akuje kuyapokea kwa bure. Mimi Yoane ninatoa maonyo haya kwa kila mutu anayesikia maneno ya unabii yanayoandikwa katika kitabu hiki: kama mutu akiongeza kitu juu ya maneno haya, Mungu atamwongezea mapigo yale yanayoandikwa katika kitabu hiki. Na kama mutu akipunguza neno kati ya maneno ya unabii yanayoandikwa katika kitabu hiki, Mungu ataondoa fungu la matunda ya muti wa uzima alilotayarishiwa, pamoja na fungu alilotayarishiwa katika ule muji mutakatifu ambavyo vimeandikwa katika kitabu hiki. Mwenye kushuhudia maneno hayo anasema: “Ndiyo, ninakuja upesi!” Amina! Kuja Ee Bwana Yesu! Ninawatakia ninyi wote neema kutoka kwa Bwana Yesu. Amina.